The Old Testament of the Holy Bible

Mwanzo 1

1 Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi. 2 Nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji; Roho ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji. 3 Mungu akasema, Iwe nuru; ikawa nuru. 4 Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema; Mungu akatenga nuru na giza. 5 Mungu akaiita nuru Mchana, na giza akaliita Usiku. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku moja. 6 Mungu akasema, Na liwe anga katikati ya maji, likayatenge maji na maji. 7 Mungu akalifanya anga, akayatenga yale maji yaliyo juu ya anga na yale maji yaliyo chini ya anga; ikawa hivyo. 8 Mungu akaliita lile anga Mbingu. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya pili. 9 Mungu akasema, Maji yaliyo chini ya mbingu na yakusanyike mahali pamoja, ili pakavu paonekane; ikawa hivyo. 10 Mungu akapaita pale pakavu Nchi; na makusanyiko ya maji akayaita Bahari; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. 11 Mungu akasema, Nchi na itoe majani, mche utoao mbegu, na mti wa matunda uzaao matunda kwa jinsi yake, ambao mbegu zake zimo ndani yake, juu ya nchi; ikawa hivyo. 12 Nchi ikatoa majani, mche utoao mbegu kwa jinsi yake, na mti uzaao matunda, ambao mbegu zake zimo ndani yake, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. 13 Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya tatu. 14 Mungu akasema, Na iwe mianga katika anga la mbingu ili itenge kati ya mchana na usiku; nayo iwe ndiyo dalili na majira na siku na miaka; 15 tena iwe ndiyo mianga katika anga la mbingu itie nuru juu ya nchi; ikawa hivyo. 16 Mungu akafanya mianga miwili mikubwa, ule mkubwa utawale mchana, na ule mdogo utawale usiku; akafanya na nyota pia. 17 Mungu akaiweka katika anga la mbingu, itie nuru juu ya nchi 18 na kuutawala mchana na usiku na kutenga nuru na giza; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. 19 Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya nne. 20 Mungu akasema, Maji na yajawe kwa wingi na kitu kiendacho chenye uhai, na ndege waruke juu ya nchi katika anga la mbingu. 21 Mungu akaumba nyangumi wakubwa, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho, ambavyo maji yalijawa navyo kwa wingi kwa jinsi zao, na kila ndege arukaye, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. 22 Mungu akavibarikia, akisema, Zaeni, mkaongezeke, mkayajaze maji ya baharini, ndege na wazidi katika nchi. 23 Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya tano. 24 Mungu akasema, Nchi na izae kiumbe hai kwa jinsi zake, mnyama wa kufugwa, nacho kitambaacho, na wanyama wa mwitu kwa jinsi zake; ikawa hivyo. 25 Mungu akafanya mnyama wa mwitu kwa jinsi zake, na mnyama wa kufugwa kwa jinsi zake, na kila kitu kitambaacho juu ya nchi kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. 26 Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi. 27 Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba. 28 Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi. 29 Mungu akasema, Tazama, nimewapa kila mche utoao mbegu, ulio juu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti, ambao matunda yake yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu; 30 na chakula cha kila mnyama wa nchi, na cha kila ndege wa angani, na cha kila kitu kitambaacho juu ya nchi, chenye uhai; majani yote ya miche, ndiyo chakula chenu; ikawa hivyo. 31 Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya sita.

Mwanzo 2

1 Basi mbingu na nchi zikamalizika, na jeshi lake lote. 2 Na siku ya saba Mungu alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe siku ya saba, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoifanya. 3 Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya. 4 Hivyo ndivyo vizazi vya mbingu na nchi zilipoumbwa. Siku ile Bwana Mungu alipoziumba mbingu na nchi 5 hapakuwa na mche wa kondeni bado, wala mboga ya kondeni haijachipuka bado, kwa maana Bwana Mungu hajainyeshea nchi mvua, wala hapana mtu wa kuilima ardhi; 6 ukungu ukapanda katika nchi, ukatia maji juu ya uso wote wa ardhi. 7 Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai. 8 Bwana Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya. 9 Bwana Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa; na mti wa uzima katikati ya bustani, na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. 10 Ukatoka mto katika Edeni wa kuitilia bustani maji, na kutokea hapo ukagawanyika kuwa vichwa vinne. 11 Jina la wa kwanza ni Pishoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Havila, ambako kuna dhahabu; 12 na dhahabu ya nchi ile ni njema; huko kuna bedola, na vito shoham. 13 Na jina la mto wa pili ni Gihoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Kushi. 14 Na jina la mto wa tatu ni Hidekeli; ndio unaopita mbele ya Ashuru. Na mto wa nne ni Frati. 15 Bwana Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza. 16 Bwana Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, 17 walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika. 18 Bwana Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye. 19 Bwana Mungu akafanyiza kutoka katika ardhi kila mnyama wa msituni, na kila ndege wa angani, akamletea Adamu ili aone atawaitaje; kila kiumbe hai, jina alilokiita Adamu likawa ndilo jina lake. 20 Adamu akawapa majina yao kila mnyama wa kufugwa, na ndege wa angani, na kila mnyama wa mwituni; lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye. 21 Bwana Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali pake, 22 na ule ubavu alioutwaa katika Adamu Bwana Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu. 23 Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume. 24 Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja. 25 Nao walikuwa uchi wote wawili, Adamu na mkewe, wala hawakuona haya.

Mwanzo 3

1 Basi nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa mwitu aliowafanya Bwana Mungu. Akamwambia mwanamke, Ati! Hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani? 2 Mwanamke akamwambia nyoka, Matunda ya miti ya bustanini twaweza kula; 3 lakini matunda ya mti ulio katikati ya bustani Mungu amesema, Msiyale wala msiyaguse, msije mkafa. 4 Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, 5 kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya. 6 Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala. 7 Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo. 8 Kisha wakasikia sauti ya Bwana Mungu, akitembea bustanini wakati wa jua kupunga; Adamu na mkewe wakajificha kati ya miti ya bustani, Bwana Mungu asiwaone. 9 Bwana Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi? 10 Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha. 11 Akasema, Ni nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je! Umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale? 12 Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala. 13 Bwana Mungu akamwambia mwanamke, Nini hili ulilolifanya? Mwanamke akasema, Nyoka alinidanganya, nikala. 14 Bwana Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu umeyafanya hayo, umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote walioko mwituni; kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako; 15 nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino. 16 Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala. 17 Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; 18 michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; 19 kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi. 20 Adamu akamwita mkewe jina lake Hawa; kwa kuwa yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai. 21 Bwana Mungu akawafanyia Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika. 22 Bwana Mungu akasema, Basi, huyu mtu amekuwa kama mmoja wetu, kwa kujua mema na mabaya; na sasa asije akanyosha mkono wake akatwaa matunda ya mti wa uzima, akala, akaishi milele; 23 kwa hiyo Bwana Mungu akamtoa katika bustani ya Edeni, ailime ardhi ambayo katika hiyo alitwaliwa. 24 Basi akamfukuza huyo mtu, akaweka Makerubi, upande wa mashariki wa bustani ya Edeni, na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.

Mwanzo 4

1 Adamu akamjua Hawa mkewe; naye akapata mimba, akamzaa Kaini, akasema, Nimepata mtoto mwanamume kwa Bwana. 2 Akaongeza akamzaa ndugu yake, Habili. Habili alikuwa mchunga kondoo, na Kaini alikuwa mkulima ardhi. 3 Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa Bwana. 4 Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. Bwana akamtakabali Habili na sadaka yake; 5 bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana. 6 Bwana akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? 7 Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde. 8 Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]Ikawa walipokuwapo uwandani,Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua. 9 Bwana akamwambia Kaini, Yuko wapi Habili ndugu yako? Akasema, Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu? 10 Akasema, Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. 11 Basi sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako; 12 utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani. 13 Kaini akamwambia Bwana, Adhabu yangu imenikulia kubwa, haichukuliki. 14 Tazama, umenifukuza leo katika uso wa ardhi, nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua. 15 Bwana akamwambia, Kwa sababu hiyo ye yote atakayemwua Kaini atalipizwa kisasi mara saba. Bwana akamtia Kaini alama, mtu amwonaye asije akampiga. 16 Kaini akatoka mbele za uso wa Bwana, akakaa katika nchi ya Nodi, mbele ya Edeni. 17 Kaini akamjua mkewe; naye akapata mimba, akamzaa Henoko; akajenga mji akauita Henoko, kwa jina la mwanawe. 18 Henoko akamzaa Iradi, Iradi akamzaa Mehuyaeli; Mehuyaeli akamzaa Methushaeli; Methushaeli akamzaa Lameki. 19 Lameki akajitwalia wake wawili, jina la wa kwanza ni Ada, na jina la wa pili ni Sila. 20 Ada akamzaa Yabali; huyo ndiye baba yao wakaao katika hema na kufuga wanyama. 21 Na jina la nduguye aliitwa Yubali; huyo ndiye baba yao wapigao kinubi na filimbi. 22 Sila naye akamzaa Tubal-kaini, mfua kila chombo cha kukatia, cha shaba na cha chuma; na umbu lake Tubal-kaini alikuwa Naama. 23 Lameki akawaambia wake zake, Sikieni sauti yangu, Ada na Sila; Enyi wake za Lameki, sikilizeni usemi wangu; Maana nimemwua mtu kwa kunitia jeraha; Kijana kwa kunichubua; 24 Kama Kaini akilipiwa kisasi mara saba, Hakika Lameki atalipiwa mara sabini na saba. 25 Adamu akamjua mke wake tena; akazaa mwana mwanamume, akamwita jina lake Sethi; maana alisema, Mungu ameniwekea uzao mwingine mahali pa Habili; kwa sababu Kaini alimwua. 26 Sethi naye akazaa mwana; akamwita jina lake Enoshi. Hapo ndipo watu walipoanza kuliitia Jina la Bwana.

Mwanzo 5

1 Hiki ndicho kitabu cha vizazi vya Adamu. Siku ile Mungu alipoumba mtu, kwa sura ya Mungu alimfanya; 2 mwanamume na mwanamke aliwaumba, akawabariki akawaita jina lao Adamu, siku ile walipoumbwa. 3 Adamu akaishi miaka mia na thelathini, akazaa mwana kwa sura yake, kwa mfano wake, akamwita jina lake Sethi. 4 Siku za Adamu baada ya kumzaa Sethi zilikuwa miaka mia nane, akazaa wana, waume na wake. 5 Siku zote za Adamu alizoishi ni miaka mia kenda na thelathini, naye akafa. 6 Sethi akaishi miaka mia na mitano, akamzaa Enoshi. 7 Sethi akaishi baada ya kumzaa Enoshi miaka mia nane na saba, akazaa wana, waume na wake. 8 Siku zote za Sethi ni miaka mia kenda na kumi na miwili, akafa. 9 Enoshi akaishi miaka tisini, akamzaa Kenani. 10 Enoshi akaishi baada ya kumzaa Kenani miaka mia nane na kumi na mitano, akazaa wana, waume na wake. 11 Siku zote za Enoshi ni miaka mia kenda na mitano, akafa. 12 Kenani akaishi miaka sabini, akamzaa Mahalaleli. 13 Kenani akaishi baada ya kumzaa Mahalaleli miaka mia nane na arobaini, akazaa wana, waume na wake. 14 Siku zote za Kenani ni miaka mia kenda na kumi, akafa. 15 Mahalaleli akaishi miaka sitini na mitano, akamzaa Yaredi. 16 Mahalaleli akaishi baada ya kumzaa Yaredi miaka mia nane na thelathini, akazaa wana, waume na wake. 17 Siku zote za Mahalaleli ni miaka mia nane na tisini na mitano, akafa. 18 Yaredi akaishi miaka mia na sitini na miwili, akamzaa Henoko. 19 Yaredi akaishi baada ya kumzaa Henoko miaka mia nane, akazaa wana, waume na wake. 20 Siku zote za Yaredi ni miaka mia kenda na sitini na miwili, akafa. 21 Henoko akaishi miaka sitini na mitano, akamzaa Methusela. 22 Henoko akaenda pamoja na Mungu baada ya kumzaa Methusela miaka mia tatu, akazaa wana, waume na wake. 23 Siku zote za Henoko ni miaka mia tatu na sitini na mitano. 24 Henoko akaenda pamoja na Mungu, naye akatoweka, maana Mungu alimtwaa. 25 Methusela akaishi miaka mia na themanini na saba, akamzaa Lameki. 26 Methusela akaishi baada ya kumzaa Lameki miaka mia saba na themanini na miwili, akazaa wana, waume na wake. 27 Siku zote za Methusela ni miaka mia kenda na sitini na kenda, akafa. 28 Lameki akaishi miaka mia na themanini na miwili, akazaa mwana. 29 Akamwita jina lake Nuhu, akinena, Huyu ndiye atakayetufariji kwa kazi yetu na kwa taabu ya mikono yetu katika nchi aliyoilaani Bwana. 30 Lameki akaishi baada ya kumzaa Nuhu miaka mia na tisini na mitano, akazaa wana, waume na wake. 31 Siku zote za Lameki ni miaka mia saba na sabini na saba, akafa. 32 Nuhu alikuwa mwenye miaka mia tano, Nuhu akawazaa Shemu, na Hamu, na Yafethi.

Mwanzo 6

1 Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, 2 wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. 3 Bwana akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini. 4 Nao Wanefili walikuwako duniani siku zile;tena ,baada ya hayo ,wana wa Mungu walipoingia kwa binti za binadamu,wakazaa nao wana;hao ndiyo waliokuwa watu hodari zamani ,watu wenye sifa. 5 Bwana akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. 6 Bwana akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo. 7 Bwana akasema, Nitamfutilia mbali mwanadamu niliyemwumba usoni pa nchi; mwanadamu na mnyama, na kitambaacho na ndege wa angani; kwa maana naghairi ya kwamba nimewafanya. 8 Lakini Nuhu akapata neema machoni pa Bwana. 9 Hivi ndivyo vizazi vya Nuhu. Nuhu alikuwa mtu wa haki, mkamilifu katika vizazi vyake; Nuhu alikwenda pamoja na Mungu. 10 Nuhu akazaa wana watatu wa kiume, Shemu, na Hamu, na Yafethi. 11 Dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma. 12 Mungu akaiona dunia, na tazama, imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani. 13 Mungu akamwambia Nuhu, Mwisho wa kila mwenye mwili umekuja mbele zangu; kwa sababu wameijaza dunia dhuluma, basi nitawaharibu pamoja na dunia. 14 Ujifanyie safina ya mti wa mvinje; fanya na vyumba ndani ya safina, ukaifunike ndani na nje kwa lami. 15 Hivi ndivyo utakavyoifanya; mikono mia tatu urefu wa safina, mikono hamsini upana wake, na mikono thelathini kwenda juu kwake. 16 Uifanyie safina mwangaza, ukaumalize juu kiasi cha mkono mmoja; ukautie mlango wa safina katika ubavu wake; ukaifanyie dari tatu, ya chini, ya pili, na ya tatu. 17 Na tazama, nitaleta gharika ya maji juu ya nchi, niharibu kila kitu chenye mwili na pumzi ya uhai, kisiwepo chini ya mbingu; kila kilichoko duniani kitakufa. 18 Lakini nitafanya agano langu nawe kuwa thabiti; nawe utaingia katika safina, wewe, na wanao, na mkeo, na wake za wanao, pamoja nawe. 19 Na katika kila kilicho hai chenye mwili, wawili wa kila namna utawaleta ndani ya safina, kuwahifadhi pamoja nawe; wawe mume na mke. 20 Katika vyote virukavyo kwa jinsi yake, na kila namna ya mnyama kwa jinsi yake, kila kitambaacho juu ya nchi kwa jinsi yake, wawili wa kila namna watakuja kwako ili uwahifadhi. 21 Ukajitwalie chakula cha kila namna kinacholika, ukakusanye, nacho kitakuwa ni chakula chenu na chao. 22 Ndivyo alivyofanya Nuhu, sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.

Mwanzo 7

1 Bwana akamwambia Nuhu, Ingia wewe na jamaa yako yote katika safina; kwa maana nimekuona wewe u mwenye haki mbele zangu katika kizazi hiki. 2 Katika wanyama wote walio safi ujitwalie saba saba, mume na mke; na katika wanyama wasio safi wawili wawili, mume na mke. 3 Tena katika ndege wa angani saba saba, mume na mke; ili kuhifadhi hai mbegu juu ya uso wa nchi yote. 4 Kwa maana baada ya siku saba nitainyeshea dunia mvua, siku arobaini mchana na usiku; na kila kilicho hai nilichokifanya juu ya uso wa nchi nitakifutilia mbali. 5 Nuhu akafanya kama vile Bwana alivyomwamuru. 6 Naye Nuhu alikuwa mtu wa miaka mia sita hapo hiyo gharika ya maji ilipokuwa juu ya nchi. 7 Nuhu akaingia katika safina, yeye, na wanawe, na mkewe, na wake za wanawe pamoja naye; kwa sababu ya maji ya gharika. 8 Na katika wanyama walio safi, na wanyama wasio safi, na ndege, navyo vyote vitambaavyo juu ya nchi, 9 wakaingia katika safina alimo Nuhu, wawili wawili, mume na mke, kama vile Mungu alivyomwamuru Nuhu. 10 Ikawa baada ya siku hizo saba, maji ya gharika yakawa juu ya nchi. 11 Katika mwaka wa mia sita wa maisha ya Nuhu, mwezi wa pili, siku ya kumi na saba ya mwezi, siku ile chemchemi zote za vilindi vikuu zilibubujika kwa nguvu, madirisha ya mbinguni yakafunguka. 12 Mvua ikanyesha juu ya nchi, siku arobaini mchana na usiku. 13 Siku ile ile Nuhu akaingia katika safina, yeye, na Shemu na Hamu na Yafethi, wana wa Nuhu, na mkewe Nuhu, na wake watatu wa wanawe pamoja naye; 14 wao na kila mnyama wa mwitu kwa jinsi yake, na kila mnyama wa kufugwa kwa jinsi yake, na kila kitambaacho, chenye kutambaa juu ya nchi, kwa jinsi yake, na kirukacho kwa jinsi yake, kila ndege wa namna yo yote. 15 Waliingia katika safina alimo Nuhu, wawili wawili, wa kila chenye mwili kilicho na pumzi ya uhai ndani yake. 16 Na walioingia, waliingia mume na mke, wa kila kitu chenye mwili, kama vile alivyomwamuru Mungu; Bwana akamfungia. 17 Ile gharika ilikuwako juu ya nchi siku arobaini; nayo maji yakazidi, yakaieleza safina, ikaelea juu ya nchi. 18 Maji yakapata nguvu, yakazidi sana juu ya nchi; na ile safina ikaelea juu ya uso wa maji. 19 Maji yakapata nguvu sana sana juu ya nchi; na milima mirefu yote iliyokuwako chini ya mbingu ikafunikizwa. 20 Maji yakapata nguvu, hata ikafunikwa milima kiasi cha mikono kumi na mitano. 21 Wakafa wote wenye mwili waendao juu ya nchi, na ndege, na wanyama wa kufugwa, na kila mnyama wa mwitu, na kila kitambaacho chenye kutambaa juu ya nchi, na kila mwanadamu; 22 kila kitu chenye pumzi ya roho ya uhai puani mwake kikafa, kila kilichokuwako katika nchi kavu. 23 Kila kilicho hai juu ya uso wa nchi kikafutiliwa mbali tangu mwanadamu hata mnyama wa kufugwa, na kitambaacho, na ndege wa angani; vilifutiliwa mbali katika nchi, akabaki Nuhu tu, na hao walio pamoja naye katika safina. 24 Maji yakapata nguvu juu ya nchi siku mia na hamsini.

Mwanzo 8

1 Na Mungu akamkumbuka Nuhu, na kila kilicho hai, na wanyama wote waliokuwamo pamoja naye katika safina; Mungu akavumisha upepo juu ya nchi, maji yakapungua; 2 chemchemi za vilindi zikafungwa, pia na madirisha ya mbinguni, mvua kutoka mbinguni ikazuiliwa; 3 maji yakadumu kuondoka katika nchi; na mwisho wa siku mia na hamsini maji yakapunguka. 4 Mwezi wa saba, siku ya kumi na saba ya mwezi, safina ikatua juu ya milima ya Ararati. 5 Maji yakapunguka-punguka hata mwezi wa kumi; mwezi huo wa kumi, siku ya kwanza ya mwezi, vilele vya milima vikaonekana. 6 Ikawa baada ya siku arobaini, Nuhu akalifungua dirisha la safina, alilolifanya; 7 akatoa kunguru, naye akatoka akaenda huko na huko, hata maji yakakauka juu ya nchi. 8 Kisha akatoa njiwa, aone kwamba maji yamepunguka usoni pa nchi; 9 bali yule njiwa hakuona mahali pa kutua kwa wayo wa mguu wake, akamrudia Nuhu safinani, maana maji yalikuwa juu ya uso wa nchi yote; naye akanyosha mkono, akamtwaa, akamwingiza mle safinani. 10 Akangoja na siku saba tena; kisha akamtoa yule njiwa katika safina mara ya pili, 11 njiwa akamjia jioni, na tazama, alikuwa na jani bichi la mzeituni kinywani mwake, ambalo amelitunda, basi Nuhu akajua ya kwamba maji yamepunguka juu ya nchi. 12 Akangoja na siku saba tena, akamtoa yule njiwa; naye asimrudie tena kamwe. 13 Ikawa mwaka wa mia sita na moja, mwezi wa kwanza, siku ya kwanza ya mwezi, maji yalikauka juu ya nchi. Nuhu akaondoa kifuniko cha safina, naye akaona, na tazama, uso wa nchi umekauka. 14 Na mwezi wa pili, siku ya ishirini na saba ya mwezi, nchi ilikuwa kavu. 15 Mungu akamwambia Nuhu, akisema, 16 Toka katika safina, wewe, na mkeo, na wanao, na wake za wanao pamoja nawe. 17 Utoe pamoja nawe kila kilicho hai kilichomo pamoja nawe, chenye mwili, ndege, na mnyama, na kila kitambaacho, chenye kutambaa juu ya nchi; wajae katika nchi, wawe na uzazi, wakaongezeke katika nchi. 18 Basi Nuhu akatoka, yeye, na wanawe, na mkewe, na wake za wanawe pamoja naye; 19 kila mnyama, na kila kitambaacho, na kila ndege, kila kinachokwenda juu ya nchi kwa kabila zao, wakatoka katika safina. 20 Nuhu akamjengea Bwana madhabahu; akatwaa katika kila mnyama aliye safi, na katika kila ndege aliye safi, akavitoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu. 21 Bwana akasikia harufu ya kumridhisha; Bwana akasema moyoni, Sitailaani nchi tena baada ya hayo kwa sababu ya wanadamu, maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake; wala sitapiga tena baada ya hayo kila kilicho hai kama nilivyofanya. 22 Muda nchi idumupo, majira ya kupanda, na mavuno, wakati wa baridi na wakati wa hari, wakati wa kaskazi na wakati wa kusi, mchana na usiku, havitakoma.

Mwanzo 9

1 Mungu akambariki Nuhu na wanawe, akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi. 2 Kila mnyama wa katika nchi atawaogopa ninyi na kuwahofu, na kila ndege wa angani: pamoja na vitu vyote vilivyojaa katika ardhi, na samaki wote wa baharini; vimetiwa mikononi mwenu. 3 Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapeni hivi vyote. 4 Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile. 5 Hakika damu yenu ya uhai wenu nitaitaka; na kwa mkono wa kila mnyama nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa ndugu ya mtu nitataka uhai wa mwanadamu. 6 Atakayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake huyo itamwagwa na mwanadamu, maana kwa mfano wake Mungu alimfanya mwanadamu. 7 Nanyi zaeni, mkaongezeke; zaeni sana katika nchi, mkaongezeke ndani yake. 8 Mungu akamwambia Nuhu, na wanawe pamoja naye, akisema, 9 Mimi, tazama, nalithibitisha agano langu nanyi; tena na uzao wenu baada yenu; 10 tena na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, ndege, na mnyama wa kufugwa, na kila mnyama wa mwitu katika nchi pamoja nanyi; wote wanaotoka katika safina, hata kila kilicho hai katika nchi. 11 Na agano langu nitalithibitisha nanyi; wala kila chenye mwili hakitafutwa tena kwa maji ya gharika; wala hakutakuwa tena gharika, baada ya hayo, kuiharibu nchi. 12 Mungu akasema, Hii ndiyo ishara ya agano nifanyalo kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, kwa vizazi vyote hata milele; 13 Mimi nauweka upinde wangu winguni, nao utakuwa ni ishara ya agano kati yangu na nchi. 14 Hata itakuwa nikitanda mawingu juu ya nchi, upinde utaonekana winguni, 15 nami nitalikumbuka agano langu, lililoko kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili, wala maji hayatakuwa gharika tena kuwaharibu wote wenye mwili. 16 Basi huo upinde utakuwa winguni; nami nitauangalia nipate kulikumbuka agano la milele lililoko kati ya Mungu na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili kilichoko katika nchi. 17 Mungu akamwambia Nuhu, Hii ndiyo ishara ya agano nililoliweka kati yangu na wote wenye mwili walioko katika nchi. 18 Wana wa Nuhu waliotoka katika safina, ni Shemu, na Hamu, na Yafethi; na Hamu ndiye baba wa Kanaani. 19 Hawa watatu walikuwa wana wa Nuhu na kwa hao nchi yote ikaenea watu. 20 Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu; 21 akanywa divai, akalewa; akawa uchi katika hema yake. 22 Hamu, baba wa Kanaani, akauona uchi wa baba yake, akawaeleza ndugu zake wawili waliokuwa nje. 23 Shemu na Yafethi wakatwaa vazi, wakalitanda mabegani mwao wote wawili, wakaenda kinyumenyume, wakaufunika uchi wa baba yao; na nyuso zao zilielekea nyuma, wala hawakuuona uchi wa baba yao. 24 Nuhu akalevuka katika ulevi wake, akajua mwana wake mdogo alivyomtendea. 25 Akasema,Na alaaniwe Kaanani;Atakuwa mtumwa kabisa kwa ndugu zake. 26 Akasema,Na atukuzwe Bwana,Mungu wa Shemu;Na kaanani awe mtumwa wake. 27 Mungu akamnafisishe Yafethi,Na akae katika hema za Shemu; Na kaanani awe mtumwa wake. 28 Na Nuhu akaishi baada ya ile gharika miaka mia tatu na hamsini. 29 Siku zote za Nuhu zilikuwa miaka mia kenda na hamsini, akafa.

Mwanzo 10

1 Hivi ndivyo vizazi vya wana wa Nuhu, Shemu, na Hamu, na Yafethi. Na kwao walizaliwa wana wa kiume baada ya gharika. 2 Wana wa Yafethi ni Gomeri, na Magogu, na Madai, na Yavani, na Tubali, na Mesheki, na Tirasi. 3 Na wana wa Gomeri ni Ashkenazi, na Rifathi, na Togama. 4 Na wana wa Yavani ni Elisha, Tarshishi, Kitimu, na Warodani. 5 Kwa hao nchi za pwani za mataifa ziligawanyikana kuwa nchi zao, kila moja kwa lugha yake, kwa jamaa zao, kufuata mataifa yao. 6 Na wana wa Hamu ni Kushi, na Misri, na Putu, na Kanaani. 7 Na wana wa Kushi ni Seba, na Havila, na Sabta, na Raama, na Sabteka. Na wana wa Raama ni Sheba, na Dedani. 8 Kushi akamzaa Nimrodi, akaanza kuwa mtu hodari katika nchi. 9 Alikuwa hodari kuwinda wanyama mbele za Bwana. Kwa hiyo watu hunena, Kama Nimrodi, hodari wa kuwinda wanyama mbele za Bwana. 10 Mwanzo wa ufalme wake ulikuwa Babeli na Ereku, na Akadi, na Kalne, katika nchi ya Shinari. 11 Akatoka katika nchi ile akaenda mpaka Ashuru, akajenga Ninawi, na Rehoboth-iri, na Kala; 12 na Reseni, kati ya Ninawi na Kala, nao ni mji mkubwa. 13 Misri akazaa Waludi, na Waanami, na Walehabi, na Wanaftuhi, 14 na Wapathrusi, na Wakasluhi; huko ndiko walikotoka Wafilisti na Wakaftori. 15 Kanaani akamzaa Sidoni, mwanawe wa kwanza, na Hethi, 16 na Myebusi, na Mwamori, na Mgirgashi, 17 na Mhivi, na Mwarki, na Msini, 18 na Mwarvadi, na Msemari, na Mhamathi. Baadaye jamaa za Wakanaani walitawanyikana. 19 Na mpaka wa Wakanaani ulianza kutoka Sidoni kwa njia ya Gerari hata Gaza; tena kwa njia ya Sodoma, na Gomora, na Adma, na Seboimu, hata Lasha. 20 Hao ndio wana wa Hamu, kufuata jamaa zao, kwa lugha zao, katika nchi zao, kufuata mataifa yao. 21 Naye Shemu ambaye ni baba wa wana wote wa Eberi, na ndugu mkubwa wa Yafethi, akazaliwa wana. 22 Wana wa Shemu ni Elamu, na Ashuru, na Arfaksadi, na Ludi, na Aramu. 23 Na wana wa Aramu ni Usi, na Huli, na Getheri, na Mashi. 24 Arfaksadi akamzaa Sela, Sela akamzaa Eberi. 25 Eberi akazaliwa wana wawili wa kiume; jina la wa kwanza ni Pelegi maana katika siku zake nchi iligawanyika; na jina la nduguye ni Yoktani. 26 Yoktani akamzaa Almodadi, na Shelefu, na Hasarmawethi, na Yera, 27 na Hadoramu, na Uzali, na Dikla, 28 na Obali, na Abimaeli, na Seba, 29 na Ofiri, na Havila, na Yobabi. Hao wote ndio wana wa Yoktani. 30 Makao yao yalikuwa kutoka Mesha kwa njia ya Sefari, mlima wa mashariki. 31 Hao ndio wana wa Shemu, kufuata jamaa zao, na lugha zao, katika nchi zao, kufuata mataifa yao. 32 Hizo ndizo jamaa za wana wa Nuhu, kufuata vizazi vyao, katika mataifa yao; na kwa hao mataifa yaligawanyika katika nchi baada ya gharika.

Mwanzo 11

1 Nchi yote ilikuwa na lugha moja na usemi mmoja. 2 Ikawa watu waliposafiri pande za mashariki waliona nchi tambarare katika nchi ya Shinari; wakakaa huko. 3 Wakaambiana, Haya, na tufanye matofali tukayachome moto. Walikuwa na matofali badala ya mawe, na lami badala ya chokaa. 4 Wakasema, Haya, na tujijengee mji, na mnara, na kilele chake kifike mbinguni, tujifanyie jina; ili tusipate kutawanyika usoni pa nchi yote. 5 Bwana akashuka ili auone mji na mnara waliokuwa wakiujenga wanadamu. 6 Bwana akasema, Tazama, watu hawa ni taifa moja, na lugha yao ni moja; na haya ndiyo wanayoanza kuyafanya, wala sasa hawatazuiliwa neno wanalokusudia kulifanya. 7 Haya, na tushuke huko, tuwachafulie usemi wao ili wasisikilizane maneno wao kwa wao. 8 Basi Bwana akawatawanya kutoka huko waende usoni pa nchi yote; wakaacha kuujenga ule mji. 9 Kwa sababu hiyo jina lake likaitwa Babeli; maana hapo ndipo Bwana alipoichafua lugha ya dunia yote; na kutoka huko Bwana akawatawanya waende usoni pa nchi yote. 10 Hivi ndivyo vizazi vya Shemu; Shemu alikuwa mtu wa miaka mia akamzaa Arfaksadi miaka miwili baada ya gharika. 11 Shemu akaishi baada ya kumzaa Arfaksadi miaka mia tano, akazaa wana, waume na wake. 12 Arfaksadi akaishi miaka thelathini na mitano, akamzaa Sela. 13 Arfaksadi akaishi baada ya kumzaa Sela miaka mia nne na mitatu, akazaa wana, waume na wake. 14 Sela akaishi miaka thelathini, akamzaa Eberi. 15 Sela akaishi baada ya kumzaa Eberi miaka mia nne na mitatu, akazaa wana, waume na wake. 16 Eberi akaishi miaka thelathini na minne, akamzaa Pelegi. 17 Eberi akaishi baada ya kumzaa Pelegi miaka mia nne na thelathini, akazaa wana, waume na wake. 18 Pelegi akaishi miaka thelathini, akamzaa Reu. 19 Pelegi akaishi baada ya kumzaa Reu miaka mia mbili na kenda, akazaa wana, waume na wake. 20 Reu akaishi miaka thelathini na miwili, akamzaa Serugi. 21 Reu akaishi baada ya kumzaa Serugi miaka mia mbili na saba, akazaa wana, waume na wake. 22 Serugi akaishi miaka thelathini, akamzaa Nahori. 23 Serugi akaishi baada ya kumzaa Nahori miaka mia mbili, akazaa wana, waume na wake. 24 Nahori akaishi miaka ishirini na kenda, akamzaa Tera. 25 Nahori akaishi baada ya kumzaa Tera miaka mia na kumi na kenda, akazaa wana, waume na wake. 26 Tera akaishi miaka sabini, akamzaa Abramu, na Nahori, na Harani. 27 Na hivi ndivyo vizazi vya Tera. Tera akamzaa Abramu, na Nahori, na Harani. Harani akamzaa Lutu. 28 Harani akafa kabla ya baba yake Tera katika nchi aliyozaliwa, yaani, katika Uru wa Wakaldayo. 29 Abramu na Nahori wakajitwalia wake. Jina la mkewe Abramu aliitwa Sarai, na jina la mkewe Nahori aliitwa Milka, binti Harani, ambaye alikuwa baba wa Milka na wa Iska. 30 Na Sarai alikuwa tasa, hakuwa na mtoto. 31 Tera akamtwaa Abramu mwanawe, na Lutu mwana wa Harani, mwana wa mwanawe, na Sarai mkwewe, mke wa Abramu mwanawe, wakatoka wote katika Uru wa Wakaldayo, waende nchi ya Kanaani, wakafika mpaka Harani wakakaa huko. 32 Siku za Tera zilikuwa miaka mia mbili na mitano; Tera akafa katika Harani.

Mwanzo 12

1 Bwana akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; 2 nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka; 3 nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa. 4 Basi Abramu akaenda, kama Bwana alivyomwamuru; Lutu akaenda pamoja naye. Naye Abramu alikuwa mtu wa miaka sabini na mitano alipotoka Harani. 5 Abramu akamchukua Sarai mkewe, na Lutu mwana wa nduguye, na vitu vyao vyote walivyokuwa wamejipatia na hao watu waliowapata huko Harani, wakatoka ili kwenda nchi ya Kanaani; nao wakaingia katika nchi ya Kanaani. 6 Abramu akapita katikati ya nchi mpaka mahali patakatifu pa Shekemu; mpaka mwaloni wa More. Na Wakanaani siku zile walikaa katika nchi hiyo. 7 Bwana akamtokea Abramu, akasema, Uzao wako nitawapa nchi hii. Naye huko akamjengea madhabahu Bwana aliyemtokea. 8 Kisha akaondoka huko akaenda mpaka mlima ulio upande wa mashariki wa Betheli, akaipiga hema yake; alikuwa na Betheli upande wa magharibi, na Ai upande wa mashariki, akamjengea Bwana madhabahu huko, akaliitia jina la Bwana. 9 Naye Abramu akasafiri, akazidi kwenda pande za kusini. 10 Basi kulikuwa njaa katika nchi ile; Abramu akashuka Misri, akae huko kwa muda maana njaa ilikuwa nzito katika nchi. 11 Ikawa alipokuwa karibu kuingia Misri, akamwambia Sarai mkewe, Tazama, najua ya kuwa u mwanamke mzuri wa uso; 12 basi itakuwa, Wamisri watakapokuona watasema, Huyu ni mkewe; kisha wataniua mimi na wewe watakuacha hai. 13 Tafadhali useme, wewe u ndugu yangu, iwe heri kwangu kwa ajili yako, na nafsi yangu iishi kwa ajili yako. 14 Basi ikawa Abramu alipofika Misri, Wamisri wakamwona huyo mwanamke ya kwamba yeye ni mzuri sana. 15 Wakuu wa Farao wakamwona, nao wakamsifu kwa Farao; basi yule mwanamke akachukuliwa nyumbani mwa Farao. 16 Naye akamtendea Abramu mema kwa ajili yake; naye alikuwa na kondoo na ng'ombe, na punda waume, na watumwa, na wajakazi, na punda wake, na ngamia. 17 Lakini Bwana akampiga Farao na nyumba yake mapigo makuu, kwa ajili ya Sarai, mkewe Abramu. 18 Ndipo Farao akamwita Abramu, akasema, N'nini hili ulilonitendea? Mbona hukuniambia ya kuwa huyo ni mkeo? 19 Mbona ulisema, Huyo ni umbu langu, hata nikamtwaa kuwa mke wangu? Basi sasa, huyo mke wako umchukue, uende zako. 20 Farao akawaagiza watu kwa ajili yake, wakampeleka njiani, na mkewe, na kila alichokuwa nacho.

Mwanzo 13

1 Abramu akapanda kutoka Misri, yeye, na mkewe, na kila alichokuwa nacho, na Lutu pamoja naye, mpaka kusini. 2 Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. 3 Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai; 4 napo ndipo palipokuwa na madhabahu aliyofanya hapo kwanza; naye Abramu akaliitia jina la Bwana hapo. 5 Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema. 6 Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja. 7 Kukawako ugomvi kati ya wachunga wanyama wa Abramu, na wachunga wanyama wa Lutu; na siku zile Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi. 8 Abramu akamwambia Lutu, Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu. 9 Je! Nchi hii yote haiko mbele yako? Basi ujitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kuume; ukienda upande wa kuume, nitakwenda upande wa kushoto. 10 Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla Bwana hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya Bwana, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. 11 Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao. 12 Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma. 13 Lakini watu wa Sodoma walikuwa wabaya, wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya Bwana. 14 Bwana akamwambia Abramu, alipokwisha kutengana na Lutu, Inua sasa macho yako, ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini, na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi; 15 maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele. 16 Na uzao wako nitaufanya uwe kama mavumbi ya nchi; hata mtu akiweza kuyahesabu mavumbi ya nchi, uzao wako nao utahesabika. 17 Ondoka, ukatembee katika nchi hii katika mapana yake, na marefu yake, maana nitakupa wewe nchi hiyo. 18 Basi Abramu akajongeza hema yake, akaja akakaa kwenye mialoni ya Mamre, nayo ni miti iliyoko Hebroni, akamjengea Bwana madhabahu huko.

Mwanzo 14

1 Ikawa siku za Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari, na Kedorlaoma mfalme wa Elamu na Tidali mfalme wa Goimu, 2 walifanya vita na Bera mfalme wa Sodoma na Birsha mfalme wa Gomora, na Shinabu mfalme wa Adma, na Shemeberi mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela, ndio Soari. 3 Hawa wote wakakutana panapo bonde la Sidimu, kwenye Bahari ya Chumvi. 4 Miaka kumi na miwili walimtumikia Kedorlaoma, hata mwaka wa kumi na tatu wakaasi. 5 Na mwaka wa kumi na nne akaja Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, wakawapiga Warefai katika Ashteroth-karnaimu, na Wazuzi katika Hamu, na Waemi katika Shawe-kiryathaimu, 6 na Wahori katika mlima wao Seiri, mpaka Elparani iliyo karibu na jangwa. 7 Kisha wakarudi wakaja mpaka Enmisfati, ndio Kadeshi, wakapiga nchi yote ya Waamaleki, na Waamori waliokaa Hasason-tamari. 8 Mfalme wa Sodoma, na mfalme wa Gomora, na mfalme wa Adma, na mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela, ndio Soari, wakatoka wakapanga vita panapo bonde la Sidimu; 9 wapigane na Kedorlaoma mfalme wa Elamu, na Tidali mfalme wa Goimu, na Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari, wafalme wanne juu ya wale watano. 10 Na bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya lami. Nao wafalme wa Sodoma na Gomora wakakimbia, wakaanguka huko, nao waliosalia wakakimbia milimani. 11 Wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na vyakula vyao vyote, wakaenda zao. 12 Wakamtwaa Lutu, mwana wa nduguye Abramu, aliyekaa huko Sodoma, na mali yake, wakaenda zao. 13 Mtu mmoja aliyeponyoka akaenda, akampasha habari Abramu Mwebrania; naye amekaa panapo mialoni ya Mamre, yule Mwamori, ndugu ya Eshkoli, na ndugu ya Aneri, na hao walikuwa wamepatana na Abramu. 14 Abramu aliposikia ya kwamba nduguye ametekwa mateka, akawapa silaha vijana wake, waliozaliwa katika nyumba yake, watu mia tatu na kumi na wanane, akawafuata mpaka Dani. 15 Akajipanga apigane nao usiku, yeye na watumwa wake, akawapiga, akawafukuza mpaka Hoba, ulioko upande wa kushoto wa Dameski. 16 Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake, na wanawake pia, na watu. 17 Abramu aliporudi kutoka kumpiga Kedorlaoma na wale wafalme waliokuwa pamoja naye, mfalme wa Sodoma akatoka amlaki katika bonde la Shawe, nalo ni Bonde la Mfalme. 18 Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana. 19 Akambariki, akasema, Abramu na abarikiwe na Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi. 20 Ahimidiwe Mungu Aliye juu sana, aliyewatia adui zako mikononi mwako. Abramu akampa fungu la kumi la vitu vyote. 21 Mfalme wa Sodoma akamwambia Abramu, Nipe mimi hao watu, na hizo mali uchukue wewe. 22 Abramu akamwambia mfalme wa Sodoma, Nimeinua mkono wangu kwa Bwana, Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi, 23 ya kuwa sitatwaa uzi wala gidamu ya kiatu wala cho chote kilicho chako, usije ukasema, Nimemtajirisha Abramu; 24 isipokuwa hivyo walivyokula vijana, na sehemu za watu waliokwenda nami, yaani, Aneri, na Eshkoli, na Mamre; na watwae wao sehemu zao.

Mwanzo 15

1 Baada ya mambo hayo neno la Bwana likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. 2 Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? 3 Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. 4 Nalo neno la Bwana likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. 5 Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. 6 Akamwamini Bwana, naye akamhesabia jambo hili kuwa haki. 7 Kisha akamwambia, Mimi ni Bwana, niliyekuleta kutoka Uru wa Wakaldayo nikupe nchi hii ili uirithi. 8 Akasema, Ee Bwana MUNGU, nipateje kujua ya kwamba nitairithi? 9 Akamwambia, Unipatie ndama wa miaka mitatu, na mbuzi mke wa miaka mitatu, na kondoo mume wa miaka mitatu, na hua, na mwana njiwa. 10 Akampatia hao wote, akawapasua vipande viwili, akaweka kila kipande kuelekea mwenzake, ila ndege hakuwapasua. 11 Hata tai walipotua juu ya mizoga Abramu akawafukuza. 12 Na jua lilipokuwa likichwa usingizi mzito ulimshika Abramu, hofu ya giza kuu ikamwangukia. 13 Bwana akamwambia Abramu, Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake, watawatumikia watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne. 14 Hata na taifa lile, watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi. 15 Lakini wewe utakwenda kwa baba zako kwa amani, utazikwa katika uzee mwema. 16 Na kizazi cha nne kitarudi hapa, maana haujatimia uovu wa Waamori bado. 17 Ikawa, jua lilipokuchwa likawa giza, tazama, tanuru ya moshi na mwenge unaowaka ulipita kati ya vile vipande vya nyama. 18 Siku ile Bwana akafanya agano na Abramu, akasema, Uzao wako nimewapa nchi hii, kutoka mto wa Misri mpaka huo mto mkubwa, mto Frati, 19 Mkeni, na Mkenizi, na Mkadmoni, 20 na Mhiti, na Mperizi, na Mrefai, 21 na Mwamori, na Mkanaani, na Mgirgashi, na Myebusi.

Mwanzo 16

1 Basi Sarai mkewe Abramu hakumzalia mwana, naye alikuwa na mjakazi, Mmisri, jina lake Hajiri. 2 Sarai akamwambia Abramu, Basi sasa, Bwana amenifunga tumbo nisizae, umwingilie mjakazi wangu labda nitapata uzao kwa yeye. Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai. 3 Sarai mkewe Abramu akamtwaa Hajiri Mmisri mjakazi wake, baada ya kukaa Abramu katika nchi ya Kanaani miaka kumi, akampa Abramu mumewe, awe mkewe. 4 Basi akamwingilia Hajiri, naye akapata mimba. Naye alipoona ya kwamba amepata mimba, bibi yake alikuwa duni machoni pake. 5 Sarai akamwambia Abramu, Ubaya ulionipata na uwe juu yako; nimekupa mjakazi wangu kifuani mwako, naye alipoona kwamba amepata mimba, mimi nimekuwa duni machoni pake. Bwana na ahukumu kati ya mimi na wewe. 6 Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. 7 Malaika wa Bwana akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. 8 Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. 9 Malaika wa Bwana akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. 10 Malaika wa Bwana akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. 11 Malaika wa Bwana akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana Bwana amesikia kilio cha mateso yako. 12 Naye atakuwa kama punda-mwitu kati ya watu, mkono wake utakuwa juu ya watu wote na mkono wa watu wote utakuwa juu yake, naye atakaa mbele yao ndugu zake wote. 13 Akaliita jina la Bwana aliyesema naye, Wewe U Mungu uonaye, kwani alisema, Hata hapa nimemwona yeye anionaye? 14 Kwa hiyo kisima kile kiliitwa Beer-lahai-roi.Tazama,kiko kati ya kadeshi na beredi. 15 Hajiri akamzalia Abramu mwana wa kiume; Abramu akamwita jina lake Ishmaeli, yule mwanawe, ambaye Hajiri alimzaa. 16 Naye Abramu alikuwa mtu wa miaka themanini na sita, hapo Hajiri alipomzalia Abramu Ishmaeli.

Mwanzo 17

1 Abramu alipokuwa mtu wa miaka tisini na kenda, Bwana akamtokea Abramu, akamwambia, Mimi ni Mungu Mwenyezi, uende mbele yangu, ukawe mkamilifu. 2 Nami nitafanya agano langu kati ya mimi na wewe, nami nitakuzidisha sana sana. 3 Abramu akaanguka kifudifudi. Mungu akamwambia, akasema, 4 Mimi, agano langu nimefanya nawe, nawe utakuwa baba wa mataifa mengi, 5 wala jina lako hutaitwa tena Abramu, lakini jina lako litakuwa Ibrahimu, kwani nimekuweka uwe baba wa mataifa mengi. 6 Nitakufanya uwe na uzao mwingi sana, nami nitakufanya kuwa mataifa, na wafalme watatoka kwako. 7 Agano langu nitalifanya imara kati ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako. 8 Nami nitakupa wewe na uzao wako baada yako nchi hii unayoikaa ugeni, nchi yote ya Kanaani, kuwa milki ya milele; nami nitakuwa Mungu wao. 9 Mungu akamwambia Ibrahimu, Nawe ulishike agano langu, wewe na uzao wako kwa vizazi vyao baada yako. 10 Hili ndilo agano langu utakalolishika, kati ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, Kila mwanamume wa kwenu atatahiriwa. 11 Mtatahiriwa nyama ya magovi yenu, na jambo hilo litakuwa ishara ya agano kati ya mimi na ninyi. 12 Mtoto wa siku nane atatahiriwa kwenu, kila mwanamume katika vizazi vyenu, mzaliwa nyumbani, na mnunuliwa kwa fedha, kila mgeni asiyekuwa wa uzao wako. 13 Mzaliwa nyumbani mwako, na mnunuliwa kwa fedha yako, lazima atahiriwe; na agano langu litakuwa katika mwili wenu, kuwa agano la milele. 14 Na mwanamume mwenye govi asiyetahiriwa nyama ya govi lake, mtu yule atatengwa na watu wake; amelivunja agano langu. 15 Mungu akamwambia Ibrahimu, Sarai mkeo, hutamwita jina lake Sarai, kwa kuwa jina lake litakuwa Sara. 16 Nami nitambariki, na tena nitakupa mwana kwake, naam, nitambariki, naye atakuwa mama wa mataifa, na wafalme wa kabila za watu watatoka kwake. 17 Ndipo Ibrahimu akaanguka kifudifudi akacheka, akasema moyoni, Je! Mtu wa umri wa miaka mia, kwake atazaliwa mtoto? Naye Sara mwenye umri wa miaka tisini atazaa? 18 Ibrahimu akamwambia Mungu, Lau kwamba Ishmaeli angeishi mbele yako. 19 Mungu akasema, Sivyo, lakini Sara mkeo atakuzalia mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Isaka. Nami nitafanya agano langu imara kwake kuwa agano la milele kwa ajili ya uzao wake baada yake. 20 Na kwa habari za Ishmaeli nimekusikia, nimembariki, nitamzidisha, nami nitamwongeza sana sana. Atazaa maseyidi kumi na wawili, nami nitamfanya awe taifa kuu. 21 Bali agano langu nitalifanya imara kwa Isaka, ambaye Sara atakuzalia majira kama haya mwaka ujao. 22 Mungu akaacha kusema naye, akapanda kutoka kwa Ibrahimu. 23 Ibrahimu akamtwaa Ishmaeli mwanawe, na wote waliozaliwa nyumbani mwake, na wote walionunuliwa kwa fedha yake, wanaume wote wa watu wa nyumba ya Ibrahimu, akawatahiri nyama ya magovi yao siku ile ile, kama Mungu alivyomwambia. 24 Naye Ibrahimu alikuwa mwenye umri wa miaka tisini na kenda alipotahiriwa nyama ya govi lake. 25 Na Ishmaeli mwanawe alikuwa mtu wa miaka kumi na mitatu, alipotahiriwa nyama ya govi lake. 26 Siku ile ile akatahiriwa Ibrahimu na Ishmaeli mwanawe. 27 Na watu wote wa nyumba yake, wazaliwa nyumbani, na wanunuliwa kwa fedha katika mkono wa mgeni, wakatahiriwa pamoja naye.

Mwanzo 18

1 Bwana akamtokea Ibrahimu karibu na mialoni ya Mamre, alipokuwa ameketi mlangoni pa hema yake mchana wakati wa hari. 2 Akainua macho yake akaona, na tazama, watu watatu wamesimama mbele yake. Naye alipowaona alipiga mbio kuwalaki kutoka mlangoni pa hema, akainama mpaka nchi, 3 akasema, Bwana wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako. 4 Na yaletwe basi maji kidogo mkanawe miguu, mkapumzike chini ya mti huu. 5 Nami nitaleta chakula kidogo, mkaburudishe moyo, baadaye mwendelee, iwapo mmemjia mtumwa wenu. Wakasema, Haya, fanya kama ulivyosema. 6 Basi Ibrahimu akaenda hima hemani kwa Sara, akasema, Himiza vipimo vitatu vya unga safi, uukande, ufanye mikate. 7 Ibrahimu akapiga mbio kwenda kundini, akaleta ndama wa ng'ombe aliye laini, mzuri, akampa mtumishi, naye akahimiza kuiandaa. 8 Akatwaa siagi na maziwa, na ndama aliyoiandaa, akawaandikia mbele yao, akasimama karibu nao chini ya mti, nao wakala. 9 Wakamwambia, Yu wapi Sara mkeo? Akasema, Yumo hemani. 10 Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume. Sara akasikia mlangoni pa hema iliyokuwapo nyuma yake. 11 Basi Ibrahimu na Sara walikuwa wazee, na umri wao mkubwa, na Sara alikuwa amekoma katika desturi ya wanawake. 12 Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee? 13 Bwana akamwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? 14 Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda Bwana? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume. 15 Akakana Sara, akisema, Sikucheka, maana aliogopa. Naye akasema, Sivyo, umecheka. 16 Kisha watu hao wakaondoka huko wakaelekeza nyuso zao Sodoma. Ibrahimu akaenda pamoja nao awasindikize. 17 Bwana akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu jambo nilifanyalo, 18 akiwa Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari, na katika yeye mataifa yote ya dunia watabarikiwa? 19 Kwa maana nimemjua ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya Bwana, wafanye haki na hukumu, ili kwamba Bwana naye akamtimizie Ibrahimu ahadi zake. 20 Bwana akasema, Kwa kuwa kilio cha Sodoma na Gomora kimezidi, na dhambi zao zimeongezeka sana, 21 basi, nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia; na kama sivyo, nitajua. 22 Basi wale watu wakatoka huko wakaelekea Sodoma; lakini Ibrahimu alikuwa akali akisimama mbele za Bwana. 23 Ibrahimu akakaribia, akasema, Je! Utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu? 24 Huenda wakawapo wenye haki hamsini katika mji, utaharibu, wala hutauacha mji kwa ajili ya hao hamsini wenye haki waliomo? 25 Hasha usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki? 26 Bwana akasema, Nikiona katika Sodoma wenye haki hamsini mjini, nitapaacha mahali pote kwa ajili yao. 27 Ibrahimu akajibu, akasema, Basi, nimeshika kusema na Bwana, nami ni mavumbi na majivu tu. 28 Huenda wakapunguka watano katika wale hamsini wenye haki, je! Utaharibu mji wote kwa kupungua watano? Akasema, Sitauharibu, nikiona humo arobaini na watano. 29 Akazidi tena kusema naye, akinena, Huenda wakaonekana humo arobaini? Akasema, Sitafanya kwa ajili ya hao arobaini. 30 Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema, Huenda wakaonekana huko thelathini? Akasema, Sitafanya, nikiona humo thelathini. 31 Akasema, Tazama, nimeshika kusema na Bwana, huenda wakaonekana huko ishirini? Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao ishirini. 32 Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema mara hii tu, Huenda wakaonekana huko kumi? Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao kumi. 33 Basi Bwana alipokwisha kuzungumza na Ibrahimu, akaenda zake; Ibrahimu naye akarudi mahali pake.

Mwanzo 19

1 Basi, wale malaika wawili wakaja Sodoma jioni; na Lutu alikuwa amekaa mlangoni pa Sodoma. Lutu akawaona akaondoka akaenda kuwalaki, akainama kifudifudi. 2 Akasema, Bwana zangu, karibuni nawasihi mwingie nyumbani mwa mtumwa wenu, mkalale, mkanawe miguu yenu, hata asubuhi mwondoke na mapema mkaende zenu. Wakasema, Sivyo, lakini tutakaa uwanjani usiku kucha. 3 Akawasihi sana, nao wakaja, wakaingia nyumbani mwake. Akawafanyia karamu, akawapikia mikate isiyochachwa nao wakala. 4 Hata kabla hawajalala, watu wa mji, wenyeji wa Sodoma, wakaizunguka nyumba, vijana kwa wazee, watu wote waliotoka pande zote. 5 Wakamwita Lutu, wakamwambia, Wa wapi wale watu waliokuja kwako usiku huu? Uwatoe kwetu, tupate kuwajua. 6 Lutu akawatokea mlangoni, akafunga mlango nyuma yake. 7 Akasema, Basi, nawasihi, ndugu zangu, msitende vibaya hivi. 8 Tazama, ninao binti wawili ambao hawajajua mtu mume, nawasihi nitawatolea kwenu mkawafanyie vilivyo vyema machoni penu, ila watu hawa msiwatende neno, kwa kuwa wamekuja chini ya dari yangu. 9 Wakasema Ondoka hapa! Kisha wakanena, Mtu huyu mmoja amekuja kwetu kuketi hali ya ugeni; naye kumbe, anataka kuhukumu! Basi tutakutenda wewe vibaya kuliko hawa. Wakamsonga sana huyo mtu, huyo Lutu, wakakaribia wauvunje mlango. 10 Lakini wale watu wakanyosha mikono yao, wakamwingiza Lutu kwao nyumbani, wakaufunga mlango. 11 Kisha wakawapiga hao watu walioko mlangoni kwa upofu, wadogo kwa wakubwa, hata wakachoka kwa kuutafuta mlango. 12 Basi wale watu wakamwambia Lutu, Je! Unaye mtu hapa zaidi? Mkwe, wanao, na binti zako, na wo wote ulio nao katika mji, uwatoe katika mahali hapa; 13 maana tutapaharibu sisi mahali hapa, kwa kuwa kilio chake kimezidi mbele za Bwana; naye Bwana ametupeleka tupaharibu. 14 Lutu akatoka akasema na wakweze, waliowaposa binti zake, akasema, Ondokeni mtoke katika mahali hapa kwa sababu Bwana atauharibu mji huu. Lakini akawa kama achezaye machoni pa wakweze. 15 Hata alfajiri ndipo malaika wakamhimiza Lutu, wakisema, Ondoka, mtwae mkeo na binti zako wawili waliopo hapa, usipotee katika maovu ya mji huu. 16 Akakawia-kawia; nao wale watu wakamshika mkono, na mkono wa mkewe, na mkono wa binti zake wawili, kwa jinsi Bwana alivyomhurumia, wakamtoa wakamweka nje ya mji. 17 Ikawa walipomtoa nje, mmoja alisema, Jiponye nafsi yako usitazame nyuma, wala usisimame katika hilo bonde po pote; ujiponye mlimani, usije ukapotea. 18 Lutu akawaambia, Sivyo, bwana wangu! 19 Tazama, mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu, nami siwezi kukimbilia mlimani nisipatwe na yale mabaya, nikafa. 20 Basi mji huu u karibu, niukimbilie, nao ni mdogo, nijiponye sasa huko, sio mdogo huu? Na nafsi yangu itaishi. 21 Akamwambia, Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili, kwamba sitauangamiza mji huo uliounena. 22 Hima, ujiponye huko, maana siwezi kufanya neno lo lote, hata uingiapo humo. Kwa hiyo jina la mji ule likaitwa Soari. 23 Jua lilikuwa limechomoza juu ya nchi Lutu alipoingia Soari. 24 Ndipo Bwana akanyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni kwa Bwana. 25 Akaangusha miji hiyo na Bonde lote, na wote waliokaa katika miji hiyo, na yote yaliyomea katika nchi ile. 26 Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi. 27 Ibrahimu akatoka asubuhi kwenda mahali aliposimama mbele za Bwana, 28 naye akatazama upande wa Sodoma na Gomora na nchi yote ya hilo Bonde, akaona, na tazama, moshi wa nchi ukapanda, kama moshi wa tanuru. 29 Ikawa Mungu alipoiharibu miji ya Bondeni, Mungu akamkumbuka Ibrahimu, akamtoa Lutu katika maangamizi alipoiangamiza miji hiyo aliyokaa Lutu. 30 Lutu akapanda kutoka Soari akakaa mlimani, na binti zake wawili pamoja naye, kwa sababu aliogopa kukaa katika Soari. Akakaa katika pango, yeye na binti zake wawili. 31 Yule mkubwa akamwambia mdogo, Baba yetu ni mzee, wala hakuna mtu mume katika nchi atuingilie kama ilivyo desturi ya dunia yote. 32 Haya, na tumnyweshe baba yetu mvinyo, tukalale naye, ili tumhifadhie baba yetu uzao. 33 Wakamnywesha baba yao mvinyo usiku ule, akaondoka huyo mkubwa akalala naye, wala yeye hana habari alipolala wala alipoondoka. 34 Ikawa siku ya pili, mkubwa akamwambia mdogo, Tazama, nimelala jana na baba yangu, tumnyweshe mvinyo tena usiku huu, ukaingie ukalale naye. 35 Wakamnywesha tena baba yao mvinyo usiku ule, akaondoka mdogo akalala naye, wala yeye hana habari alipolala wala alipoondoka. 36 Basi hao binti wote wawili wa Lutu wakapata mimba kwa baba yao. 37 Yule mkubwa akazaa mwana, akamwita jina lake Moabu; huyo ndiye baba wa Wamoabi, hata leo. 38 Na yule mdogo naye akazaa mwana akamwita jina lake Benami; huyo ndiye baba wa Waamoni hata leo.

Mwanzo 20

1 Ibrahimu akaondoka huko kwenda nchi ya kusini, akakaa kati ya Kadeshi na Shuri, naye akatembea katika Gerari. 2 Ibrahimu akamnena Sara mkewe, Huyu ni ndugu yangu. Basi Abimeleki mfalme wa Gerari akapeleka watu akamtwaa Sara. 3 Lakini Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto ya usiku, akamwambia, Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, maana ni mkewe mtu. 4 Basi Abimeleki alikuwa hakumkaribia, akasema, Ee Bwana, Je! Utaua hata taifa lenye haki? 5 Je! Hakuniambia mwenyewe, Huyu ni ndugu yangu? Na mwanamke mwenyewe naye alisema, Huyu ni ndugu yangu. Kwa ukamilifu wa moyo wangu, na kwa kuwa safi mikono yangu, nimefanya hivi. 6 Mungu akamwambia katika ndoto, Nami nimejua ya kwamba kwa ukamilifu wa moyo wako umefanya hivi, ndipo nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse. 7 Basi sasa umrudishe mwanamke kwa mtu huyo, maana yeye ni nabii, naye atakuombea, upate kuishi. Bali usipomrudisha, fahamu ya kwamba kwa hakika utakufa wewe na watu wote ulio nao. 8 Abimeleki akaamka asubuhi na mapema, akawaita watumwa wake wote, akawaambia maneno hayo yote masikioni mwao, nao watu hao wakaogopa sana. 9 Kisha Abimeleki akamwita Ibrahimu, akamwambia, Umetutenda nini? Nimekukosa nini, hata ukaleta juu yangu na juu ya ufalme wangu dhambi kuu? Umenitenda matendo yasiyotendeka. 10 Abimeleki akamwambia Ibrahimu, Umeona nini hata ukatenda jambo hili? 11 Ibrahimu akasema, Kwa sababu naliona, Yakini hapana hofu ya Mungu mahali hapa, nao wataniua kwa ajili ya mke wangu. 12 Naye kweli ni ndugu yangu, binti wa baba yangu ila siye mwana wa mama yangu, ndipo akawa mke wangu. 13 Ikawa hapo Mungu aliponisafirisha kutoka nyumba ya baba yangu, nikamwambia, Hii ndiyo fadhili yako, utakayonifanyia. Kila mahali tuingiapo, useme, Huyu ni ndugu yangu. 14 Basi Abimeleki akatwaa kondoo, na ng'ombe, na watumwa, na wajakazi, akampa Ibrahimu, akamrudishia Sara mkewe. 15 Abimeleki akasema, Nchi yangu iko mbele yako, kaa upendapo. 16 Naye akamwambia Sara, Tazama! Nimempa ndugu yako fedha elfu, itakuwa kifunika macho kwako mbele ya wote walio pamoja nawe, nawe utakuwa na haki mbele ya watu wote. 17 Ibrahimu akamwomba Mungu, Mungu akamponya Abimeleki, na mkewe, na wajakazi wake, nao wakazaa wana. 18 Maana Bwana alikuwa ameyafunga matumbo ya watu wa nyumbani mwa Abimeleki, wasizae, kwa ajili ya Sara mkewe Ibrahimu.

Mwanzo 21

1 Bwana akamjia Sara kama alivyonena, na Bwana akamfanyia kama alivyosema. 2 Sara akapata mimba akamzalia Ibrahimu mwana wa kiume katika uzee wake, kwa muhula alioambiwa na Mungu. 3 Ibrahimu akamwita jina lake Isaka, yule mwana aliyezaliwa, ambaye Sara alimzalia. 4 Ibrahimu akamtahiri Isaka mwanawe, alipokuwa mwenye siku nane, kama Mungu alivyomwamuru. 5 Naye Ibrahimu alikuwa mtu wa miaka mia, alipozaliwa mwana wake Isaka. 6 Sara akasema, Mungu amenifanyia kicheko; kila asikiaye atacheka pamoja nami. 7 Akasema, N'nani angemwambia Ibrahimu, Sara atanyonyesha wana? Maana nimemzalia mwana katika uzee wake. 8 Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya. 9 Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. 10 Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka. 11 Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. 12 Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa. 13 Naye mwana wa mjakazi nitamfanya kuwa taifa, maana huyu naye ni uzao wako. 14 Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. 15 Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. 16 Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. 17 Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. 18 Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. 19 Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. 20 Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde. 21 Akakaa katika jangwa la Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri. 22 Ikawa wakati ule Abimeleki, na Fikoli mkuu wa jeshi lake, wakamwambia Ibrahimu, wakinena, Mungu yu pamoja nawe katika yote unayotenda. 23 Basi sasa uniapie kwa Mungu, ya kuwa hutanitenda hila, wala mwanangu, wala mjukuu wangu, lakini kwa kadiri ya fadhili niliyokutendea utanitendea mimi, na nchi hii ambayo umetembea ndani yake. 24 Ibrahimu akasema, Nitaapa. 25 Kisha Ibrahimu akamlaumu Abimeleki kwa sababu ya kisima cha maji ambacho watumwa wa Abimeleki wamekinyang'anya. 26 Abimeleki akasema, Mimi sijui ni nani aliyetenda neno hili, wala hukuniambia, wala sikusikia habari hii ila leo tu. 27 Ibrahimu akatwaa kondoo na ng'ombe akampa Abimeleki, na hao wawili wakafanya mapatano. 28 Ibrahimu akaweka wana kondoo wa kike saba peke yao. 29 Abimeleki akamwambia Ibrahimu, Hawa wana kondoo wa kike saba, uliowaweka peke yao, maana yake nini? 30 Akasema, Hawa wana kondoo wa kike saba utawapokea mkononi mwangu, wawe ushuhuda ya kuwa ni mimi niliyekichimba kisima hiki. 31 Kwa hiyo akapaita mahali pale Beer-sheba, kwa sababu waliapa huko wote wawili. 32 Basi wakafanya mapatano huko Beer-sheba. Abimeleki, na Fikoli mkuu wa jeshi lake, wakaondoka wakarudi hata nchi ya Wafilisti. 33 Ibrahimu akapanda mkwaju huko Beer-sheba, akaliitia huko jina la Bwana Mungu wa milele. 34 Ibrahimu akakaa hali ya ugeni katika nchi ya Wafilisti siku nyingi.

Mwanzo 22

1 Ikawa baada ya mambo hayo Mungu alimjaribu Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. 2 Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia. 3 Ibrahimu akaondoka alfajiri, akatandika punda wake, akachukua vijana wawili pamoja naye, na Isaka mwanawe, akachanja kuni kwa ajili ya hiyo sadaka ya kuteketezwa, akaondoka, akaenda mpaka mahali alipoambiwa na Mungu. 4 Siku ya tatu Ibrahimu akainua macho yake, akapaona mahali pakali mbali. 5 Ibrahimu akawaambia vijana wake, Kaeni ninyi hapa pamoja na punda, na mimi na kijana tutakwenda kule, tukaabudu, na kuwarudia tena. 6 Basi Ibrahimu akazitwaa kuni za hiyo sadaka, akamtwika Isaka mwanawe; akatwaa moto na kisu mkononi mwake, wakaenda wote wawili pamoja. 7 Isaka akasema na Ibrahimu baba yake, akinena, Babangu! Naye akasema, Mimi hapa, mwanangu. Akasema, Tazama! Moto upo, na kuni zipo, lakini yuko wapi mwana-kondoo kwa sadaka ya kuteketezwa? 8 Ibrahimu akasema, Mungu atajipatia mwana-kondoo kwa hiyo sadaka, mwanangu. Basi wakaendelea wote wawili pamoja. 9 Wakafika mahali pale alipoambiwa na Mungu, Ibrahimu akajenga madhabahu huko, akaziweka tayari kuni, kisha akamfunga Isaka mwanawe, akamweka juu ya madhabahu, juu ya zile kuni. 10 Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe. 11 Ndipo malaika wa Bwana akamwita kutoka mbinguni, akasema, Ibrahimu! Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. 12 Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee. 13 Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe. 14 Ibrahimu akapaita mahali hapo Yehova-yire,kama watu wasemavyo hata leo,Katika mlima wa BWANA itapatikana. 15 Malaika wa Bwana akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni 16 akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema Bwana, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, 17 katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; 18 na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu. 19 Basi Ibrahimu akawarudia vijana wake, wakaondoka, wakaenda zao pamoja mpaka Beer-sheba; Ibrahimu akakaa huko Beer-sheba. 20 Ikawa baada ya mambo hayo, Ibrahimu akaambiwa ya kwamba, Tazama, Milka naye amemzalia Nahori ndugu yako wana; 21 Usi, mzaliwa wa kwanza wake, na Buzi nduguye, na Kemueli, baba wa Aramu; 22 na Kesedi, na Hazo, na Pildashi, na Yidlafu, na Bethueli. 23 Bethueli akamzaa Rebeka; hao wanane Milka alimzalia Nahori ndugu wa Ibrahimu. 24 Na suria wake Reuma naye alizaa Teba na Gahamu na Tahashi na Maaka.

Mwanzo 23

1 Basi umri wake Sara ulikuwa miaka mia na ishirini na saba ndio umri wake Sara. 2 Sara akafa katika Kiriath-arba, ndio Hebroni, katika nchi ya Kanaani. Ibrahimu akaja kumlilia Sara na kumwombolezea. 3 Akaondoka Ibrahimu kutoka mbele ya maiti wake, akasema na wazawa wa Hethi, akinena, 4 Mimi ni mgeni, ninatembea kwenu; nipeni mahali pa kuzikia kwenu, pawe pangu, nimzike maiti wangu atoke mbele yangu. 5 Wazawa wa Hethi wakamjibu Ibrahimu, wakamwambia, 6 Utusikie, Ee bwana, ndiwe mtu mkuu sana kwetu, uzike maiti wako katika kaburi lile utakalochagua katika makaburi yetu. Hapana mtu kwetu atakayekuzuilia kaburi lake, usizike maiti wako. 7 Ibrahimu akaondoka, akainama mbele ya watu wa nchi, mbele ya hao wazawa wa Hethi. 8 Naye akazungumza nao, akisema, Ikiwa nia yenu nimzike maiti wangu atoke mbele yangu, mnisikie, mkaniombee kwa Efroni bin Sohari, 9 ili kwamba anipe pango ya Makpela, iliyo katika mpaka wa shamba lake, na anipe kwa kima kilicho kamili, katikati yenu, iwe milki yangu ya kuzikia. 10 Basi Efroni alikuwa akiketi kati ya wazawa wa Hethi. Efroni Mhiti akamjibu Ibrahimu, na wazawa wa Hethi wanasikiliza, hata watu wote waingiao mlango wa mji wake, akisema, 11 Sivyo, bwana wangu, unisikilize. Lile shamba nakupa, na pango iliyomo nakupa; mbele ya wana wa watu wangu nakupa, uzike maiti wako. 12 Ibrahimu akainama mbele ya watu wa nchi. 13 Akamwambia Efroni, na watu wa nchi wanasikiliza, akisema, Tafadhali unisikilize; nitatoa kima cha shamba, nawe ukipokee kwangu, nami nitamzika humo maiti wangu. 14 Efroni akamjibu Ibrahimu, akamwambia, 15 Bwana wangu, unisikilize. Sehemu ya nchi, ambayo thamani yake ni shekeli za fedha mia nne, n'nini hii baina yako na yangu? Basi uzike maiti wako. 16 Ibrahimu akakubali maneno ya Efroni. Ibrahimu akampimia Efroni ile fedha aliyotaja masikioni mwa wazawa wa Hethi, shekeli za fedha mia nne za namna inayotumika na wenye biashara. 17 Basi shamba la Efroni lililokuwa katika Makpela kuelekea Mamre, shamba, na pango iliyokuwamo, na miti yote iliyokuwamo shambani, iliyokuwa katika mipaka yake pande zote, vyote viliyakinishwa 18 kuwa mali yake Ibrahimu, mbele ya wazawa wa Hethi, mbele ya watu wote waingiao katika mlango wa mji wake. 19 Basi baada ya hayo Ibrahimu akamzika Sara mkewe katika pango ya shamba la Makpela kuelekea Mamre, ndiyo Hebroni, katika nchi ya Kanaani. 20 Na lile shamba, na pango iliyomo, iliyakinishwa kuwa mali yake Ibrahimu na wazawa wa Hethi, kuwa mahali pa kuzikia.

Mwanzo 24

1 Basi Ibrahimu alikuwa mzee mwenye miaka mingi, na Bwana alikuwa amembariki Ibrahimu katika vitu vyote. 2 Ibrahimu akamwambia mtumishi wake, mzee wa nyumba yake, aliyetawala vitu vyake vyote, Tafadhali uutie mkono wako chini ya paja langu, 3 nami nitakuapisha kwa Bwana, Mungu wa mbingu, na Mungu wa nchi, kwamba hutamtwalia mwanangu mke katika binti za Wakanaani ambao nakaa kati yao; 4 bali enenda hata nchi yangu, na kwa jamaa zangu, ukamtwalie mwanangu Isaka mke. 5 Yule mtumishi akamwambia, Labda yule mwanamke hatakubali kufuatana nami mpaka nchi hii, je! Nimrudishe mwanao mpaka nchi ulikotoka? 6 Ibrahimu akamwambia, Ujihadhari, usimrudishe mwanangu huko. 7 Bwana, Mungu wa mbingu, aliyenitoa katika nyumba ya babangu, na kusema nami katika nchi niliyozaliwa, aliniapia akisema, Nitawapa uzao wako nchi hii; yeye atampeleka malaika wake mbele yako, nawe utamtwalia mwanangu mke tokea huko; 8 na yule mwanamke asipokubali kufuatana nawe, basi, utafunguliwa kiapo changu hiki; lakini usimrudishe mwanangu huko. 9 Yule mtumishi akaweka mkono wake chini ya paja la Ibrahimu bwana wake, akamwapia katika neno hilo. 10 Kisha huyo mtumishi akatwaa ngamia kumi katika ngamia za bwana wake akaenda zake, maana mali zote za bwana wake zilikuwa mkononi mwake, akaondoka, akaja mpaka Mesopotamia, mpaka mji wa Nahori. 11 Akawapigisha magoti ngamia nje ya mji karibu na kisima cha maji wakati wa jioni, wakati ambapo wanawake wanakwenda kuteka maji. 12 Naye akasema, Ee Bwana, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, nakuomba mambo yangu uyajalie yawe heri leo, ukamfadhili bwana wangu Ibrahimu. 13 Tazama! Nimesimama karibu na kisima cha maji, na binti za watu wa mjini wanatoka kuteka maji, 14 basi na iwe hivi; yule msichana nitakayemwambia, Tua mtungi wako, nakuomba, ninywe; naye akasema, Unywe, nami nitawanywesha na ngamia zako pia; basi huyu na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako Isaka; na kwa hayo nitajua ya kuwa umemfadhili bwana wangu. 15 Ikawa, kabla hajaisha kunena, tazama, Rebeka anatokea, binti wa Bethueli mwana wa Milka, mkewe Nahori, ndugu wa Ibrahimu, naye ana mtungi begani pake. 16 Naye yule msichana alikuwa mzuri sana uso wake, bikira, wala mwanamume hajamjua bado; akashuka kisimani, akajaza mtungi wake, akapanda. 17 Ndipo yule mtumishi akapiga mbio kwenda kumlaki, akasema, Tafadhali unipe maji kidogo katika mtungi wako ninywe. 18 Naye akasema, Unywe, bwana wangu, akafanya haraka, akatua mtungi wake mkononi mwake, akamnywesha. 19 Hata alipokwisha kumnywesha akasema, Na ngamia zako nitawatekea, hata watakapokwisha kunywa. 20 Akafanya haraka, akamwaga maji ya mtungi wake katika birika, akapiga mbio kisimani ateke, akawatekea ngamia zake wote. 21 Basi yule mtu akamkazia macho, akanyamaza, ili ajue kwamba Bwana ameifanikisha safari yake ama sivyo. 22 Ikawa, ngamia walipokwisha kunywa, yule mtu akatwaa pete ya dhahabu, uzani wake ulikuwa nusu shekeli, na vikuku viwili kwa mikono yake, uzani wake ulikuwa shekeli kumi za dhahabu, 23 akasema, U binti wa nani wewe? Tafadhali uniambie. Je! Iko nafasi katika nyumba ya baba yako tupate mahali pa kukaa kwa muda? 24 Akasema, Mimi ni binti wa Bethueli mwana wa Milka, aliyemzalia Nahori. 25 Tena akamwambia, Kwetu kuna majani na malisho ya kutosha, na mahali pa kukaa wageni. 26 Yule mtu akainama akamsujudu Bwana. 27 Akasema, Na atukuzwe Bwana, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, ambaye hakuacha rehema zake na kweli yake kwa bwana wangu. Bwana akaniongoza mimi nami njiani hata nyumba ya nduguze bwana wangu. 28 Basi yule msichana akapiga mbio, akawaambia watu wa nyumba ya mama yake mambo hayo. 29 Na Rebeka alikuwa na kaka, jina lake Labani. Labani akatoka mbio kumwendea yule mtu kisimani. 30 Ikawa, alipoiona ile pete, na vikuku mikononi mwa nduguye, akasikia maneno ya Rebeka nduguye, akisema, Hivyo ndivyo alivyoniambia mtu huyo, basi akamjia mtu yule, na tazama, amesimama karibu na ngamia kisimani. 31 Akasema, Karibu, wewe uliyebarikiwa na Bwana, mbona unasimama nje? Kwa maana nimeiweka nyumba tayari, na nafasi kwa ngamia. 32 Na mtu yule akaingia katika nyumba, akawafungua ngamia; naye akatoa majani na malisho kwa ngamia, na maji ya kuoshea miguu yake, na miguu ya watu waliokuwa pamoja naye. 33 Akaandaliwa chakula, lakini akasema, Sili mpaka niseme kwanza maneno yangu. Akamwambia, Haya, sema. 34 Akasema, Mimi ni mtumwa wa Ibrahimu, 35 na Bwana amembarikia sana bwana wangu, amekuwa mtu mkuu; amempa kondoo, na ng'ombe, na fedha, na dhahabu, na watumwa, na wajakazi, na ngamia, na punda. 36 Naye Sara, mkewe bwana wangu, akamzalia bwana wangu mwana wa kiume, katika uzee wake; naye amempa yote aliyo nayo. 37 Kisha bwana wangu akaniapisha akisema, Usimtwalie mwanangu mke wa binti za Wakanaani, ambao nakaa katika nchi yao. 38 Ila uende mpaka nyumbani kwa babangu, na kwa jamaa zangu, ukamtwalie mwanangu mke. 39 Nikamwambia bwana wangu, Labda huyo mwanamke hatafuatana nami. 40 Akaniambia, Bwana, ambaye naenenda machoni pake, atapeleka malaika wake pamoja nawe, atafanikisha njia yako; nawe umtwalie mwanangu mke katika jamaa zangu, na wa nyumba ya babangu. 41 Ndipo utafunguliwa kiapo changu hapo utakapowafikilia jamaa zangu; nao wasipokupa msichana huyo, utafunguliwa kiapo changu. 42 Nami nikaja leo kisimani, nikasema, Ee Bwana, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, ukinifanikishia sasa njia yangu niendayo mimi, 43 tazama! Nimesimama karibu na kisima cha maji; basi na iwe hivi, msichana ajaye kuteka maji, nikamwambia, Nipe, nakuomba, maji kidogo katika mtungi wako ninywe, 44 naye akaniambia, Unywe wewe, na ngamia zako pia nitawatekea, huyo na awe ndiye mke Bwana aliyemwekea mwana wa bwana wangu. 45 Hata kabla sijaisha kusema moyoni mwangu, tazama! Rebeka akatokea, na mtungi begani mwake. Akashuka kisimani akateka. Nami nikamwambia, Tafadhali nipe maji ninywe. 46 Akafanya haraka akatua mtungi wake chini, akanena, Unywe, na ngamia zako nitawanywesha pia; basi nikanywa, akawanywesha na ngamia nao. 47 Kisha nikamwuliza nikasema, U binti wa nani wewe? Naye akasema, Mimi ni binti Bethueli, mwana wa Nahori, Milka aliyemzalia. Nami nikamtia hazama puani mwake na vikuku mikononi mwake. 48 Nikainama, nikamsujudia Bwana, nikamtukuza Bwana, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, aliyeniongoza njiani, nimtwalie mwana wa bwana wangu binti wa ndugu yake. 49 Basi, kama mnataka kumfanyia rehema na kweli bwana wangu, niambieni kama sivyo, niambieni; ili nigeuke upande wa kuume au wa kushoto. 50 Ndipo Labani na Bethueli wakajibu wakasema, Neno hili limetoka kwa Bwana, wala sisi hatuwezi kukuambia neno jema wala baya. 51 Tazama, huyo Rebeka yuko mbele yako, umchukue, ukaende zako awe mke wa mwana wa bwana wako, kama alivyosema Bwana. 52 Ikawa mtumishi wa Ibrahimu aliposikia maneno yao, akainama hata nchi mbele za Bwana. 53 Kisha huyo mtumishi akatoa vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na mavazi, akampa Rebeka; na vitu vya thamani akampa nduguye na mamaye pia. 54 Wakala wakanywa, yeye na watu waliokuwa pamoja naye, nao wakakaa usiku. Wakaondoka asubuhi, naye akasema, Nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu. 55 Ndugu yake na mama yake wakasema, Msichana na akae kwetu kama siku kumi, zisipungue, baadaye aende. 56 Naye akawaambia, Msinikawilishe, mradi Bwana amefanikisha njia yangu; nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu. 57 Wakasema, Na tumwite huyo msichana, tumwulize mwenyewe. 58 Wakamwita Rebeka wakamwuliza, Je! Utakwenda na mtu huyu? Akasema, Nitakwenda. 59 Ndipo wakampeleka Rebeka ndugu yao, na yaya wake, na mtumishi wa Ibrahimu, na watu wake. 60 Wakambarikia Rebeka, wakamwambia, Ndugu yetu, uwe wewe mama wa kumi elfu, mara elfu nyingi, na wazao wako waurithi mlango wa hao wawachukiao. 61 Rebeka akaondoka na vijakazi wake, nao wakapanda juu ya ngamia, wakamfuata yule mtu. Naye huyo mtumishi akamchukua Rebeka akaenda zake. 62 Basi Isaka alikuwa amekuja kwa njia ya Beer-lahai-roi, maana alikaa katika nchi ya kusini. 63 Isaka akatoka ili kutafakari kondeni wakati wa jioni; akainua macho yake, akaona, kuna ngamia wanakuja. 64 Rebeka akainua macho, naye alipomwona Isaka, alishuka juu ya ngamia. 65 Akamwambia mtumishi, Ni nani mtu huyu ajaye kondeni kutulaki? Mtumishi akasema, Huyu ndiye bwana wangu. Basi akatwaa shela yake akajifunika. 66 Yule mtumishi akamwambia Isaka mambo yote aliyoyatenda. 67 Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake.

Mwanzo 25

1 Ibrahimu alioa mke mwingine jina lake akiitwa Ketura. 2 Akamzalia Zimrani, na Yokshani, na Medani, na Midiani, na Ishbaki, na Sua. 3 Yokshani akamzaa Sheba, na Dedani; na wana wa Dedani walikuwa Waashuri na Waletushi, na Waleumi. 4 Na wana wa Midiani walikuwa, Efa, na Eferi, na Hanoki, na Abida, na Eldaa. Hao wote walikuwa ni wana wa Ketura. 5 Ibrahimu akampa Isaka yote aliyokuwa nayo. 6 Lakini wana wa masuria aliokuwa nao Ibrahimu, Ibrahimu akawapa zawadi, naye akawaondoa katika mahali alipokaa Isaka mwanawe, wakati wa uhai wake, waende pande za mashariki, mpaka nchi ya Kedemu. 7 Hizi ndizo siku za miaka ya maisha ya Ibrahimu alizoishi, miaka mia, na sabini na mitano. 8 Ibrahimu akafariki, naye akafa katika uzee mwema, mzee sana, ameshiba siku, akakusanyika kwa watu wake. 9 Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango ya Makpela, katika shamba la Efroni bin Sohari Mhiti, lielekealo Mamre. 10 Katika lile shamba alilolinunua Ibrahimu kwa wazawa Hethi, huko ndiko alikozikwa Ibrahimu na Sara mkewe. 11 Ikawa, baada ya kufa kwake Ibrahimu, Mungu akambariki Isaka mwanawe. Naye Isaka akakaa karibu ya Beer-lahai-roi. 12 Hivi ndivyo vizazi vya Ishmaeli, mwana wa Ibrahimu, ambaye Hajiri, Mmisri, mjakazi wa Sara, alimzalia Ibrahimu. 13 Na haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kwa majina yao, na kwa vizazi vyao. Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, ni Nebayothi, na Kedari, na Abdeeli, na Mibsamu, 14 na Mishma, na Duma, na Masa, 15 na Hadadi, na Tema, na Yeturi, na Nafishi, na Kedema. 16 Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ni majina yao, katika miji yao, na katika vituo vyao, maseyidi kumi na wawili kwa kufuata jamaa zao. 17 Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka mia na thelathini na saba. Akakata roho, akafa, akakusanyika kwa watu wake. 18 Wakakaa toka Havila mpaka Shuri, unaoelekea Misri, kwa njia ya kwenda Ashuru. Akakaa katikati ya ndugu zake wote. 19 Na hivi ndivyo vizazi vya Isaka, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka. 20 Isaka akawa mwenye miaka arobaini alipomtwaa Rebeka binti Bethueli, Mshami, wa Padan-aramu, ndugu wa Labani, Mshami, kuwa mke wake. 21 Isaka akamwomba Bwana kwa ajili ya mke wake, maana alikuwa tasa. Naye Bwana akamwitikia, na Rebeka mkewe akachukua mimba. 22 Watoto wakashindana tumboni mwake. Naye akasema, Ikiwa ni hivi, kuishi kwanifaa nini? Akaenda kumwuliza Bwana. 23 Bwana akamwambia,Mataifa mawili yamo tumboni mwako,Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako.Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili,Na mkubwa atamtumikia mdogo. 24 Siku zake za kuzaa zilipotimia, tazama! Mapacha walikuwamo tumboni mwake. 25 Wa kwanza akatoka, naye alikuwa mwekundu mwili wote kama vazi la nywele. Wakamwita jina lake Esau. 26 Baadaye ndugu yake akatoka, na mkono wake unamshika Esau kisigino. Akaitwa jina lake Yakobo. Isaka alikuwa mwenye miaka sitini mkewe alipowazaa. 27 Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na Yakobo alikuwa mtu mtulivu, mwenye kukaa hemani. 28 Basi Isaka akampenda Esau, kwa sababu alikula mawindo yake, na Rebeka akampenda Yakobo. 29 Yakobo akapika chakula cha dengu. Esau akaja kutoka nyikani, naye alikuwa amechoka sana. 30 Esau akamwambia Yakobo, Tafadhali, unipe hicho chakula chekundu nile, kwa kuwa ninazimia mimi. Kwa hiyo walimwita jina lake Edomu. 31 Yakobo akamwambia, Kwanza niuzie leo haki yako ya mzaliwa wa kwanza. 32 Esau akasema, Tazama, mimi ni karibu kufa, itanifaa nini haki hii ya uzazi? 33 Yakobo akamwambia, Uniapie kwanza. Naye akamwapia, akamwuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza. 34 Yakobo akampa Esau mkate na chakula cha dengu, naye akala, akanywa, kisha akaondoka, akaenda zake. Hivyo Esau akaidharau haki yake ya mzaliwa wa kwanza.

Mwanzo 26

1 Ikawa njaa katika nchi hiyo, mbali na njaa ile ya kwanza iliyokuwa siku za Ibrahimu. Isaka akamwendea Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, huko Gerari. 2 Bwana akamtokea, akasema, Usishuke kwenda Misri, kaa katika nchi nitakayokuambia. 3 Kaa ugenini katika nchi hiyo, nami nitakuwa pamoja nawe, na kukubariki, maana nitakupa wewe na uzao wako nchi hizi zote. Nami nitakifanya imara kiapo nilichomwapia Ibrahimu baba yako. 4 Nitazidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, nami nitawapa uzao wako nchi hizi zote, na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia. 5 Kwa sababu Ibrahimu alisikia sauti yangu, akayahifadhi maagizo yangu, na amri zangu, na hukumu zangu, na sheria zangu. 6 Isaka akakaa katika Gerari. 7 Watu wa mahali hapo wakamwuliza habari za mkewe. Akasema, Ni ndugu yangu huyu maana aliogopa kusema, Ni mke wangu, watu wa nchi wasije wakamwua kwa ajili ya Rebeka; kwa maana alikuwa mzuri wa uso. 8 Ikawa alipokuwa amekaa huko siku nyingi, Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, akachungulia dirishani, akamwona Isaka anacheza-cheza na Rebeka mkewe. 9 Abimeleki akamwita Isaka, akasema, Yakini huyu ni mkeo, mbona ulisema, Ni ndugu yangu huyu? Isaka akamwambia, Kwa sababu nalisema, Nisife kwa ajili yake. 10 Abimeleki akasema, Ni nini hii uliyotutendea? Labda mtu mmojawapo angalilala na mkeo bila kufikiri, nawe ungalitutia hatiani. 11 Basi Abimeleki akawaamuru watu wote, akisema, Amgusaye mtu huyu au mkewe lazima atauawa. 12 Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, Bwana akambariki. 13 Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. 14 Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. 15 Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. 16 Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. 17 Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. 18 Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. 19 Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. 20 Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. 21 Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. 22 Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi. 23 Akapanda kutoka hapo mpaka Beer-sheba. 24 Bwana akamtokea usiku uleule, akasema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu baba yako, usiogope, maana mimi ni pamoja nawe, nami nitakubarikia, na kuzidisha uzao wako kwa ajili ya Ibrahimu mtumishi wangu. 25 Akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la Bwana. Akapiga hema yake huko, na watumwa wa Isaka wakachimba kisima huko. 26 Ndipo Abimeleki akamwendea kutoka Gerari, pamoja na Ahuzathi rafiki yake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake. 27 Isaka akawauliza, Mbona mwanijia, nanyi mmenichukia, mkanifukuza kwenu? 28 Wakasema, Hakika tuliona ya kwamba Bwana alikuwa pamoja nawe; nasi tukasema, Na tuapiane, sisi na wewe, na kufanya mapatano nawe 29 ya kuwa hutatutenda mabaya, iwapo sisi hatukukugusa wewe, wala hatukukutendea ila mema, tukakuacha uende zako kwa amani; nawe sasa u mbarikiwa wa Bwana. 30 Basi akawafanyia karamu, nao wakala, wakanywa. 31 Wakaondoka asubuhi na mapema, wakaapiana wao kwa wao, kisha Isaka akawapa ruhusa, nao wakaenda zao kwa amani. 32 Ikawa siku ileile, watumwa wa Isaka wakaja wakampasha habari za kile kisima walichokuwa wamekichimba, wakamwambia, Tumeona maji. 33 Naye akakiita jina lake Shiba; kwa hiyo jina la mji huo ni Beer-sheba, hata leo. 34 Esau alipokuwa mwenye miaka arobaini, akamwoa Yudithi, binti Beeri, Mhiti, na Basemathi, binti Eloni, Mhiti. 35 Roho zao Isaka na Rebeka zikajaa uchungu kwa ajili yao.

Mwanzo 27

1 Ikawa Isaka alipokuwa mzee, na macho yake yamepofuka asione, akamwita Esau, mwanawe mkubwa, akamwambia, Mwanangu. Naye akamwitikia, Mimi hapa. 2 Akasema, Tazama, sasa mimi nimekuwa mzee, wala sijui siku ya kufa kwangu. 3 Basi, nakuomba, chukua mata yako, podo lako na upinde wako, ukaende nyikani uniwindie mawindo; 4 ukanifanyie chakula kitamu namna ile niipendayo, ukaniletee, ili nile; na roho yangu ikubariki, kabla sijafa. 5 Na Rebeka akasikia, Isaka aliposema na Esau mwanawe. Basi Esau akaenda nyikani awinde mawindo, ayalete. 6 Rebeka akamwambia Yakobo mwanawe, akisema, Angalia, nimemsikia baba yako akisema na Esau, ndugu yako, akinena, 7 Niletee mawindo, ukanifanyie chakula kitamu ili nile, na kukubariki mbele za Bwana kabla ya kufa kwangu. 8 Basi, mwanangu, sikiliza sauti yangu kama nitakavyokuagiza. 9 Enenda sasa kundini ukanitwalie wana-mbuzi wawili walio wema, nami nitawafanya chakula kitamu kwa baba yako, namna ile aipendayo. 10 Kisha utampelekea baba yako, apate kula, ili akubariki kabla ya kufa kwake. 11 Yakobo akamwambia Rebeka mamaye, Esau ndugu yangu ni mtu mwenye malaika, na mimi ni mtu laini. 12 Labda baba yangu atanipapasa, nami nitakuwa machoni pake kama mdanganyifu; nami nitaleta juu yangu laana wala si mbaraka. 13 Mamaye akamwambia, Laana yako na iwe juu yangu, mwanangu, usikie sauti yangu tu, enenda ukaniletee wana-mbuzi. 14 Akaenda, akawatwaa, akamletea mamaye. Mamaye akafanya chakula kitamu namna ile aliyopenda babaye. 15 Kisha Rebeka akatwaa mavazi mazuri ya Esau mwanawe mkubwa, aliyokuwa nayo nyumbani, akamvika Yakobo mwanawe mdogo. 16 Na ngozi za wana-mbuzi akamvika mikononi, na katika ulaini wa shingo yake. 17 Naye akampa Yakobo mwanawe mikononi mwake hicho chakula kitamu, na mkate alioufanya. 18 Akaja kwa baba yake, akasema, Babangu. Akasema, Mimi hapa, U nani wewe, mwanangu? 19 Yakobo akamwambia babaye, Mimi ni Esau, mzaliwa wako wa kwanza, nimefanya kama ulivyoniambia. Ondoka, tafadhali, ukae kitako, ule mawindo yangu, ili roho yako inibariki. 20 Isaka akamwuliza mwanawe, Imekuwaje umepata upesi namna hii, mwanangu? Akasema, Kwa sababu Bwana, Mungu wako, amenifanikisha. 21 Isaka akamwambia Yakobo, Karibu, tafadhali, ili nikupapase, mwanangu, nione kwamba wewe ndiwe mwanangu Esau, ama siyo. 22 Basi Yakobo akamkaribia Isaka, babaye, naye akampapasa, akasema, Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau. 23 Wala hakumtambua, kwa maana mikono yake ilikuwa kama mikono ya Esau, ndugu yake, yenye malaika; basi akambariki. 24 Akamwuliza, Wewe ndiwe kweli mwanangu Esau? Akasema, Ndimi. 25 Akasema, Niletee karibu nami nipate kula mawindo ya mwanangu, ili roho yangu ikubariki. Akamsogezea karibu, naye akala; kisha akamletea mvinyo, akanywa. 26 Isaka, baba yake, akamwambia, Njoo karibu sasa, ukanibusu, mwanangu. 27 Akakaribia akambusu. Naye akasikia harufu ya mavazi yake, akambariki akasema, Tazama, harufu ya mwanangu Ni kama harufu ya shamba alilolibariki Bwana. 28 Mungu na akupe ya umande wa mbingu, Na ya manono ya nchi, Na wingi wa nafaka na mvinyo. 29 Mataifa na wakutumikie Na makabila wakusujudie, Uwe bwana wa ndugu zako, Na wana wa mama yako na wakusujudie. Atakayekulaani alaaniwe, Na atakayekubariki abarikiwe. 30 Ikawa Isaka alipokwisha kumbariki Yakobo, na alipokuwa Yakobo ndiyo kwanza ametoka mbele ya Isaka, baba yake, mara Esau ndugu yake akaja kutoka katika kuwinda kwake. 31 Naye pia amefanya chakula kitamu akamletea babaye, akamwambia baba yake. Babangu na aondoke, ale mawindo ya mwanawe, ili roho yako inibariki. 32 Isaka, baba yake, akamwuliza, U nani wewe? Akasema, Mimi ni mwanao, Esau, mzaliwa wako wa kwanza. 33 Isaka akatetemeka tetemeko kuu sana, akasema, Ni nani basi yule aliyetwaa mawindo akaniletea? Nami nimekwisha kula kabla hujaja wewe, nikambariki; naam, naye atabarikiwa. 34 Esau aliposikia maneno ya babaye, akalia kilio kikubwa cha uchungu sana, akamwambia babaye, Nibariki na mimi, mimi nami, Ee babangu. 35 Akasema, Nduguyo amekuja kwa hila, akauchukua mbaraka wako. 36 Akasema, Je! Hakuitwa Yakobo kwa haki, maana amejitia mahali pangu mara mbili hizi? Alichukua haki yangu ya mzaliwa wa kwanza, na sasa amechukua mbaraka wangu. Akasema, Je! Hukuniwekea na mimi mbaraka? 37 Isaka akajibu, akamwambia Esau, Tazama, nimemfanya awe bwana wako, na ndugu zake wote nimempa kuwa watumishi wake; kwa nafaka na mvinyo nimemtegemeza, nami nikufanyie nini sasa, mwanangu? 38 Esau akamwambia babaye, Una mbaraka mmoja tu, babangu? Unibariki mimi, mimi nami, Ee babangu. Esau akapaza sauti yake, akalia. 39 Isaka, baba yake, akajibu, akamwambia,Angalia,penye manono ya nchi patakuwa makao yako,Na penye umande wa mbingu unaotoka juu. 40 Kwa upanga wako wewe utaishi, nawe utamtumikia nduguyo; Na itakuwa utakapoponyoka, Utalivunja kongwa lake katika shingo yako. 41 Esau akamchukia Yakobo kwa ajili ya ule mbaraka babaye aliombarikia. Esau akasema moyoni mwake, Siku za kumlilia baba yangu zinakaribia, ndipo nitakapomwua ndugu yangu Yakobo. 42 Rebeka akaarifiwa maneno ya Esau, mwanawe mkubwa. Akapeleka mtu kumwita Yakobo, mwanawe mdogo, akamwambia, Tazama, katika habari zako Esau, ndugu yako, anajifariji moyo wake, maana anakusudia kukuua. 43 Na sasa, mwanangu, sikia sauti yangu, uondoke, ukimbilie kwa Labani, ndugu yangu huko Harani; 44 ukae kwake siku chache, hata ghadhabu ya ndugu yako igeuke; 45 hata ikuondokee ghadhabu ya ndugu yako, akasahau uliyomtenda. Ndipo nitakapopeleka watu kukuchukua kutoka huko. Kwa nini nifiwe nanyi nyote wawili siku moja? 46 Rebeka akamwambia Isaka, Rohoni mwangu sina raha kwa sababu ya hao binti za Hethi. Kama Yakobo akitwaa mke katika binti za Hethi, kama hawa binti za nchi, maisha yangu yatanifaidia nini?

Mwanzo 28

1 Basi Isaka akamwita Yakobo, akambariki, akamwagiza akamwambia, Usitwae mke wa binti za Kanaani. 2 Ondoka, uende Padan-aramu, mpaka nyumba ya Bethueli baba ya mama yako, ukajitwalie huko mke katika binti za Labani, ndugu wa mama yako. 3 Na Mungu Mwenyezi, akubariki, akuzidishe, na kukuongeza, ili uwe mkutano wa makabila. 4 Akupe mbaraka wa Ibrahimu, wewe na uzao wako pamoja nawe, upate kuirithi nchi ya kusafiri kwako, Mungu aliyompa Ibrahimu. 5 Basi Isaka akampeleka Yakobo, naye akaenda Padan-aramu, kwa Labani, mwana wa Bethueli, Mshami, ndugu wa Rebeka, mama yao Yakobo na Esau. 6 Esau akaona ya kwamba Isaka amembariki Yakobo na kumpeleka Padan-aramu, ili ajitwalie mke huko, na katika kumbariki akamwagiza, akasema, Usitwae mke wa binti za Kanaani, 7 na ya kuwa Yakobo amewatii babaye na mamaye, akaenda Padan-aramu. 8 Esau akaona ya kuwa binti za Kanaani hawakumpendeza Isaka, baba yake. 9 Basi Esau akaenda kwa Ishmaeli akamtwaa Mahalathi, binti Ishmaeli mwana wa Ibrahimu, ndugu wa Nebayothi, kuwa mkewe pamoja na wakeze aliokuwa nao. 10 Yakobo akatoka Beer-sheba, kwenda Harani. 11 Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale. 12 Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake. 13 Na tazama, Bwana amesimama juu yake, akasema, Mimi ni Bwana, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako. 14 Na uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi, na mashariki, na kaskazini, na kusini; na katika wewe, na katika uzao wako, jamaa zote za dunia watabarikiwa. 15 Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia. 16 Yakobo akaamka katika usingizi wake, akasema, Kweli Bwana yupo mahali hapa, wala mimi sikujua. 17 Naye akaogopa akasema, Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka, hapa ni nyumba ya Mungu, napo ndipo lango la mbinguni. 18 Yakobo akaondoka asubuhi na mapema, akalitwaa lile jiwe aliloliweka chini ya kichwa chake, akalisimamisha kama nguzo, na kumimina mafuta juu yake. 19 Akaita jina la mahali pale Betheli; lakini jina la mji ule hapo kwanza uliitwa Luzu. 20 Yakobo akaweka nadhiri akisema, Mungu akiwa pamoja nami, akinilinda katika njia niiendeayo, na kunipa chakula nile, na nguo nivae; 21 nami nikirudi kwa amani nyumbani kwa baba yangu, ndipo Bwana atakuwa Mungu wangu. 22 Na jiwe hili nililolisimamisha kama nguzo litakuwa nyumba ya Mungu; na katika kila utakalonipa hakika nitakutolea wewe sehemu ya kumi.

Mwanzo 29

1 Kisha Yakobo akashika njia yake, akafika nchi ya wana wa mashariki. 2 Naye akaangalia, na tazama, kiko kisima kondeni, na makundi matatu ya kondoo yamelala karibu nacho, kwa sababu katika kisima kile hunywesha makundi; na palikuwa na jiwe kubwa juu ya kinywa cha kisima. 3 Makundi yote hukusanyika huko, watu wakafingirisha hilo jiwe katika kinywa cha kisima wakawanywesha kondoo, na kulirudisha jiwe juu ya kinywa cha kisima mahali pake. 4 Yakobo akawauliza, Ndugu zangu, watu wa wapi ninyi? Wakasema, Tu wa Harani sisi. 5 Akawauliza, Je! Mnamjua Labani, mwana wa Nahori? Wakasema, Tunamjua. 6 Akawauliza, Je! Hajambo? Wakasema, Hajambo; tazama, Raheli binti yake anakuja na kondoo. 7 Akasema, Tazama, ukali mchana bado, wala sio wakati wa kukusanya wanyama; wanywesheni kondoo, mwende kuwalisha. 8 Wakasema, Hatuwezi, hata yakusanyike makundi yote, watu wakafingirishe jiwe katika kinywa cha kisima, ndipo tunapowanywesha kondoo. 9 Hata alipokuwa akisema nao, Raheli akaja na kondoo za baba yake, maana aliwachunga. 10 Ikawa Yakobo alipomwona Raheli binti Labani, ndugu wa mamaye, na kondoo za Labani, ndugu wa mamaye, Yakobo akakaribia, na kulifingirisha lile jiwe litoke katika kinywa cha kisima, akawanywesha kondoo za Labani, ndugu wa mamaye. 11 Yakobo akambusu Raheli, akainua sauti yake akalia. 12 Yakobo akamwarifu Raheli ya kuwa yeye ni ndugu wa babaye, na ya kuwa ni mwana wa Rebeka. Basi akapiga mbio akampasha babaye habari. 13 Ikawa Labani aliposikia habari za Yakobo, mwana wa nduguye, akaenda mbio amlaki, akamkumbatia, akambusu, akamleta nyumbani kwake. Naye akamwambia Labani maneno hayo yote. 14 Labani akamwambia, Ndiwe kweli mfupa wangu na nyama yangu. Naye akakaa kwake muda wa mwezi mmoja. 15 Labani akamwambia Yakobo, Kwa sababu wewe ni ndugu yangu, basi, je! Unitumikie bure? Niambie mshahara wako utakuwa nini? 16 Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. 17 Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. 18 Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. 19 Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu. 20 Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. 21 Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. 22 Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu. 23 Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. 24 Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. 25 Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? 26 Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; 27 timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine. 28 Yakobo akafanya hivi, akatimiza siku zake saba. Naye akampa Raheli binti yake kuwa mkewe. 29 Labani akampa binti yake Raheli mjakazi wake Bilha, awe mjakazi wake. 30 Akaingia kwa Raheli naye, akampenda Raheli kuliko Lea, akatumika kwa ajili yake miaka saba mingine. 31 Bwana akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai. 32 Lea akapata mimba akazaa mwana, akampa jina lake, Reubeni, maana alisema, Kwa kuwa Bwana ameona teso langu; sasa mume wangu atanipenda. 33 Akapata mimba tena akazaa mwana, akasema, Kwa kuwa Bwana amesikia ya kwamba mimi sikupendwa, amenipa na huyu; akamwita jina lake Simeoni. 34 Akapata mimba tena, akazaa mwana, akasema, Basi wakati huu mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu. Kwa hiyo akamwita jina lake Lawi. 35 Akapata mimba tena, akazaa mwana. Akasema, Mara hii nitamsifu Bwana; kwa hiyo akamwita jina lake Yuda; akaacha kuzaa.

Mwanzo 30

1 Naye Raheli alipoona ya kuwa hamzalii Yakobo mwana, Raheli alimwonea ndugu yake wivu. Akamwambia Yakobo, Nipe wana; kama sivyo, nitakufa mimi. 2 Yakobo akamghadhibikia Raheli, akasema, Je! Mimi ni badala ya Mungu, aliyekuzuilia uzao wa mimba? 3 Akasema, Yuko mjakazi wangu, Bilha, uingie kwake ili kwamba azae juu ya magoti yangu, nami nipate uzao kwa yeye. 4 Basi akampa Bilha mjakazi wake kuwa mkewe. Yakobo akaingia kwake. 5 Naye Bilha akapata mimba, akamzalia Yakobo mwana. 6 Raheli akasema, Mungu amenipa haki yangu, naye amesikia sauti yangu, akanipa mwana. Kwa hiyo akamwita jina lake Dani. 7 Bilha, mjakazi wa Raheli, akapata mimba tena, akamzalia Yakobo mwana wa pili. 8 Raheli akasema, Kwa mashindano makuu nimeshindana na ndugu yangu, nikashinda. Akamwita jina lake Naftali. 9 Lea alipoona ya kuwa ameacha kuzaa, alimtwaa Zilpa, mjakazi wake, akampa Yakobo kuwa mkewe. 10 Zilpa, mjakazi wa Lea, akamzalia Yakobo mwana. 11 Lea akasema, Bahati njema! Akamwita jina lake Gadi. 12 Zilpa, mjakazi wa Lea, akamzalia Yakobo mwana wa pili. 13 Lea akasema, Ni heri mimi, maana wanawake wataniita heri. Akamwita jina lake Asheri. 14 Reubeni akaenda siku za mavuno ya ngano akaona tunguja kondeni, akazileta kwa Lea mamaye. Ndipo Raheli akamwambia Lea, Nipe mimi baadhi ya tunguja za mwanao. 15 Naye akamwambia, Je! Ni jambo dogo kuninyang'anya mume wangu; hata wataka kuzitwaa tunguja za mwanangu pia? Raheli akamwambia, Kwa hiyo atalala kwako usiku huu kwa tunguja za mwanao. 16 Yakobo akaja kutoka kondeni jioni, Lea akatoka kumlaki, akasema, Lazima uje kwangu, kwa sababu nimekuajiri, kwa tunguja za mwanangu; akalala kwake usiku ule. 17 Mungu akamsikia Lea, naye akapata mimba, akamzalia Yakobo mwana wa tano. 18 Lea akasema, Mungu amenipa ujira wangu, kwa sababu nimempa mume wangu mjakazi wangu. Akamwita jina lake Isakari. 19 Lea akapata mimba tena, akamzalia Yakobo mwana wa sita. 20 Lea akasema, Mungu amenipa mahari njema, sasa mume wangu atakaa nami, kwa kuwa nimemzalia wana sita. Akamwita jina lake Zabuloni. 21 Baadaye akazaa binti, akamwita jina lake Dina. 22 Mungu akamkumbuka Raheli; Mungu akamsikia, akamfungua tumbo. 23 Akapata mimba, akazaa mwana, akasema, Mungu ameondoa aibu yangu. 24 Akamwita jina lake Yusufu, akisema, Bwana aniongeze mwana mwingine. 25 Ikawa Raheli alipomzaa Yusufu, Yakobo akamwambia Labani, Nipe ruhusa niende kwetu, na kwenye nchi yangu. 26 Nipe wake zangu na watoto wangu, niliokutumikia, niende zangu, maana umejua utumishi wangu niliokutumikia. 27 Labani akamwambia, Iwapo nimeona fadhili machoni pako, kaa, maana nimetambua ya kwamba Bwana amenibariki kwa ajili yako. 28 Akasema, Sema mshahara wako utakao, nami nitatoa. 29 Akamwambia, Umejua jinsi nilivyokutumikia, na jinsi wanyama wako walivyokuwa kwangu. 30 Maana mali yako ilikuwa haba kabla sijaja, nayo imezidi kuwa nyingi, Bwana akakubariki kila nilikokwenda. Basi sasa, nitaangalia lini mambo ya nyumba yangu mwenyewe? 31 Akamwuliza, Nikupe nini? Yakobo akasema, Usinipe kitu; ukinifanyia neno hili, nitalisha wanyama wako tena na kuwalinda. 32 Nitapita katika wanyama wako wote leo, na kutoa huko kila mnyama aliye na madoadoa na marakaraka, na kila mnyama mweusi katika hao kondoo, na aliye na marakaraka na madoadoa katika mbuzi; nao watakuwa mshahara wangu. 33 Na haki yangu itanishuhudia katika siku zijazo, utakapokuja kwa habari ya mshahara wangu ulioko kwako. Kila asiye madoadoa au marakaraka katika mbuzi, au asiye mweusi katika kondoo, akionekana kwangu, itahesabiwa kuwa ameibiwa. 34 Labani akasema, Tazama, na iwe hivi kama usemavyo. 35 Basi akatoa siku ile mbuzi waume walio na milia na madoadoa, na mbuzi wake walio na madoadoa na marakaraka, kila aliye na doa jeupe, na kondoo wote waliokuwa weusi, akawatia mikononi mwa wanawe. 36 Akajitenga na Yakobo mwendo wa siku tatu; naye Yakobo akachunga wanyama wa Labani waliosalia. 37 Yakobo akatwaa fito za mlubna mbichi, na mlozi, na mwaramoni, akazibambua maganda, mistari myeupe ionekane ndani ya hizo fito. 38 Akazisimamisha fito hizo alizozibambua katika mabirika ya kunyweshea maji, pale walipokuja wanyama wanywe; wakachukua mimba walipokuja kunywa. 39 Wanyama wakapata mimba mbele ya hizo fito, wakazaa wanyama walio na milia, na madoadoa, na marakaraka. 40 Na Yakobo akawatenga wana-kondoo, akazielekeza nyuso za makundi zielekee wale waliokuwa na milia, na kila aliyekuwa mweusi katika wanyama wa Labani. Akaweka kando wanyama wake mwenyewe, wala hakuwachanganya pamoja na wanyama wa Labani. 41 Ikawa kila walipopata mimba wanyama wenye nguvu, Yakobo akaziweka zile fito mbele ya macho ya hao wanyama katika mabirika ili kwamba wachukue mimba kati ya zile fito, 42 lakini wanyama walipodhoofika hakuziweka zile fito. Basi wale dhaifu walikuwa wa Labani, na wenye nguvu walikuwa wa Yakobo. 43 Kwa hiyo mtu huyo akazidi mno, akawa na wanyama wengi, na vijakazi, na watumwa, na ngamia, na punda.

Mwanzo 31

1 Basi Yakobo akasikia maneno ya wana wa Labani, wakisema, Yakobo amechukua mali yote ya baba yetu; na kwa mali ya baba yetu amepata fahari hii yote. 2 Yakobo akaona uso wa Labani, ya kuwa hakumtazama vema kama jana na juzi. 3 Bwana akamwambia Yakobo, Urudi mpaka nchi ya baba zako na kwa jamaa zako, nami nitakuwa pamoja nawe. 4 Yakobo akatuma watu, akawaita Raheli na Lea waje nyikani kwenye wanyama wake. Akawaambia, 5 Naona uso wa baba yenu, kwamba hanitazami vema kama jana na juzi. Lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami. 6 Nanyi mmejua ya kwamba kwa nguvu zangu zote nimemtumikia baba yenu. 7 Na baba yenu amenidanganya, akabadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hakumwacha kunidhuru. 8 Aliposema, Walio na madoadoa watakuwa mshahara wako, wanyama wote wakazaa madoadoa. Aliposema, Walio na milia watakuwa mshahara wako, ndipo wanyama wote wakazaa wenye milia. 9 Hivi Mungu akamnyang'anya mali yake baba yenu, na kunipa mimi. 10 Ikawa, wakati wale wanyama walipochukua mimba, naliinua macho yangu nikaona katika ndoto, na tazama, mabeberu waliowapanda hao wanyama walikuwa na milia, na madoadoa, na marakaraka. 11 Na malaika wa Mungu akaniambia katika ndoto, Yakobo! Nikasema, Mimi hapa. 12 Akasema, Inua, basi, macho yako, ukaone; mabeberu wote wanaopanda wanyama wana milia, na madoadoa, na marakaraka; maana nimeona yote aliyokutendea Labani. 13 Mimi ni Mungu wa Betheli, huko ulikotia mafuta nguzo, na kuniwekea nadhiri. Sasa ondoka, toka katika nchi hii, urudi mpaka nchi ile uliyozaliwa. 14 Raheli na Lea wakajibu, wakamwambia, Je! Imetubakia sehemu au urithi katika nyumba ya baba yetu? 15 Hakutufanya kama wageni, maana ametuuza, naye amekula fedha zetu kabisa? 16 Maana mali yote ambayo Mungu amemnyang'anya baba yetu, mali hiyo ndiyo yetu na ya wana wetu. Basi yo yote Mungu aliyokuambia, uyafanye. 17 Ndipo Yakobo akaondoka, akapandisha wanawe na wakeze juu ya ngamia. 18 Akachukua wanyama wake wote, na mali yake yote aliyokuwa ameyapata, na wanyama aliowapata katika Padan-aramu, ili afike kwa Isaka babaye katika nchi ya Kanaani. 19 Basi Labani alikuwa amekwenda kuwakata manyoya kondoo zake, na Raheli akaviiba vinyago vya babaye. 20 Yakobo akamhadaa Labani, Mshami, kwa kuwa hakumwambia ya kwamba anakimbia. 21 Basi akakimbia yeye na yote aliyokuwa nayo; akaondoka akauvuka mto, akaelekeza uso wake kwenda mlima wa Gileadi. 22 Hata siku ya tatu Labani akaambiwa ya kwamba Yakobo amekimbia, 23 akatwaa ndugu zake pamoja naye, akamfuata mwendo wa siku saba. Akampata katika mlima wa Gileadi. 24 Mungu akamjia Labani, Mshami, katika ndoto ya usiku, akamwambia, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. 25 Labani akamfikia Yakobo, na Yakobo alikuwa amepiga hema zake katika mlima, na Labani na ndugu zake wakapiga hema zao katika mlima wa Gileadi. 26 Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. 27 Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? 28 Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu. 29 Ninao uwezo mkononi mwangu wa kukufanyia madhara; lakini Mungu wa baba yako usiku huu ameniambia, akisema, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. 30 Basi sasa, umetoka kwa sababu umetamani sana nyumba ya baba yako. Mbona basi umeiiba miungu yangu? 31 Yakobo akajibu, akamwambia Labani, Kwa sababu naliogopa, nikasema, Usije ukaninyang'anya binti zako kwa nguvu. 32 Awaye yote utakayemwona kuwa nayo miungu yako, yeye asiishi. Mbele ya ndugu zetu ukitambue kilicho chako kwangu, ukakichukue. Maana Yakobo hakujua ya kwamba Raheli ameiiba. 33 Labani akaingia katika hema ya Yakobo, na hema ya Lea, na hema ya vijakazi wawili, wala hakuiona. Akatoka katika hema ya Lea, akaingia katika hema ya Raheli. 34 Basi Raheli alikuwa amevitwaa vile vinyago ameviweka katika matandiko ya ngamia, na kuvikalia. Labani akapapasa hema yote wala hakuviona. 35 Naye Raheli akamwambia babaye, Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike. Akatafuta, wala hakuviona vile vinyago. 36 Yakobo akakasirika, akagombana na Labani. Yakobo akajibu, akamwambia Labani, N'nini hatia yangu? Nayo ni nini dhambi yangu, hata ukanifuatia namna hii? 37 Umepapasa-papasa vyombo vyangu vyote; ni kitu gani ulichokiona cha nyumbani mwako? Kiweke hapa mbele ya ndugu zangu, na ndugu zako, wakaamue kati yetu. 38 Miaka hii ishirini nimekaa kwako; kondoo zako wala mbuzi zako wake hawakuharibu mimba wala waume katika wanyama wako sikuwala. 39 Kilichoraruliwa na hayawani sikukuletea, mimi mwenyewe nimetwaa hasara yake, wewe umekidai katika mkono wangu, ikiwa kilichukuliwa mchana, au ikiwa kilichukuliwa usiku. 40 Hii ilikuwa hali yangu; mchana jua likanipata, na baridi usiku, usingizi ukanitoka machoni mwangu. 41 Miaka hii ishirini nimekaa nyumbani mwako; nilikutumikia miaka kumi na minne kwa binti zako wawili, na miaka sita kwa wanyama wako, nawe umebadili mshahara wangu mara kumi. 42 Kama Mungu wa baba yangu, Mungu wa Ibrahimu na Hofu ya Isaka, hangalikuwa pamoja nami, hakika sasa ungalinifukuza mikono mitupu. Mateso yangu na kazi za mikono yangu Mungu ameziona, akakukemea usiku huu. 43 Labani akajibu, akamwambia Yakobo, Hao binti ni binti zangu, na wana ni wanangu, na wanyama ni wanyama wangu, na yote uyaonayo ni yangu; nami naweza kuwatendea nini leo binti zangu na wana wao waliowalea? 44 Haya! Na tufanye agano, mimi na wewe, liwe kwa ushahidi kati ya mimi na wewe. 45 Yakobo akatwaa jiwe akalisimamisha kama nguzo. 46 Yakobo akawaambia ndugu zake, Kusanyeni mawe. Wakatwaa mawe, wakafanya chungu, nao wakala huko karibu na ile chungu. 47 Labani aliiita Yegarsahadutha, lakini Yakobo aliiita Galedi. 48 Labani akasema, Chungu hii ni shahidi kati ya mimi na wewe hivi leo. Kwa hiyo likaitwa jina lake Galedi, 49 na Mispa, maana alisema, Mungu avizie kati ya mimi na wewe, wakati tusipoonana. 50 Ukiwatesa binti zangu, na ukitwaa wake zaidi ya binti zangu, wala hapana mtu pamoja nasi, tazama, Mungu ni shahidi kati ya mimi na wewe. 51 Labani akamwambia Yakobo, Tazama chungu hii utazame na nguzo niliyoitia kati ya mimi na wewe. 52 Chungu hii na iwe shahidi, na nguzo hii na iwe shahidi, ya kuwa mimi sitapita chungu hii kuja kwako, wala wewe hutapita chungu hii na nguzo hii uje kwangu, kwa madhara. 53 Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Nahori, Mungu wa baba yao, ahukumu kati yetu. 54 Yakobo akachinja sadaka katika mlima, akawaita ndugu zake waje wale chakula, nao wakala chakula, wakakaa usiku kucha mlimani. 55 Labani akaondoka asubuhi na mapema, akawabusu wanawe na binti zake, akawabariki; kisha Labani akaenda zake, akarudi kwao.

Mwanzo 32

1 Yakobo akashika njia yake na malaika wa Mungu wakakutana naye. 2 Naye Yakobo alipowaona, alisema, Hili ni jeshi la Mungu. Akapaita mahali pale, Mahanaimu. 3 Basi, Yakobo akapeleka wajumbe mbele yake kwenda kwa Esau nduguye mpaka nchi ya Seiri katika nyika ya Edomu. 4 Akawaagiza akisema, Mwambieni hivi bwana wangu, Esau, Hivi ndivyo asemavyo mtumwa wako, Yakobo; Nimekaa ugenini kwa Labani, na kukawia huko hata sasa, 5 nami nina ng'ombe, na punda, na kondoo, na watumwa, na vijakazi; nami nimepeleka watu nimpashe bwana wangu habari, nipate neema machoni pako. 6 Wale wajumbe wakarudi kwa Yakobo wakisema, Tulifika kwa ndugu yako, Esau, naye anakuja kukulaki, na watu mia nne pamoja naye. 7 Ndipo Yakobo akaogopa sana, na kufadhaika sana, akawagawanya watu waliopo pamoja naye, na kondoo, na ng'ombe, na ngamia, wawe matuo mawili. 8 Akasema, Akija Esau kwa kundi la kwanza, akalipiga, kundi litakalosalia litaokoka. 9 Yakobo akasema, Ee Mungu wa baba yangu Ibrahimu, na Mungu wa baba yangu Isaka, Bwana, uliyeniambia, Rudi uende mpaka nchi yako, na kwa jamaa zako, nami nitakutendea mema; 10 mimi sistahili hata kidogo hizo rehema zote na kweli yote uliyomfanyia mtumwa wako; maana nalivuka mto huo wa Yordani na fimbo yangu tu, na sasa nimekuwa matuo mawili. 11 Uniokoe sasa na mkono wa ndugu yangu, mkono wa Esau, maana mimi namwogopa, asije akanipiga, na mama pamoja na wana. 12 Nawe ulisema, Hakika nitakutendea mema, nami nitafanya uzao wako uwe kama mchanga wa bahari, usiohesabika kwa kuwa mwingi. 13 Akakaa huko usiku ule. Kisha akatwaa baadhi ya vitu alivyokuwa navyo, kuwa zawadi kwa Esau, nduguye; 14 mbuzi wake mia mbili, na mbuzi waume ishirini, kondoo wake mia mbili, na kondoo waume ishirini; 15 ngamia wanyonyeshao thelathini pamoja na wana wao, ng'ombe wake arobaini na mafahali kumi; punda wake ishirini na wana wao kumi. 16 Akawatia mkononi mwa watumwa wake, kila kundi peke yake. Naye akawaambia watumwa wake, Vukeni mbele yangu, mkaache nafasi kati ya kundi na kundi. 17 Akamwagiza yule wa kwanza akasema, Esau, ndugu yangu, akikukuta, na kukuuliza, akisema, Wewe u wa nani? Unakwenda wapi? Tena ni wa nani hawa walio mbele yako? 18 Basi, useme, Ni wa mtumwa wako, Yakobo, ni zawadi, aliyompelekea bwana wangu, Esau. Na tazama, yeye mwenyewe yuko nyuma yetu. 19 Akamwagiza tena wa pili, na wa tatu, wote waliofuata makundi, akisema, Hivi ndivyo mtakavyomwambia Esau, akiwakuta. 20 Tena semeni, Tazama, mtumwa wako, Yakobo, yuko nyuma yetu. Maana alisema, Nitamsuluhisha kwa zawadi inayonitangulia, baadaye nitamwona uso wake; huenda atanikubali uso wangu. 21 Basi ile zawadi ikavuka mbele yake, naye mwenyewe akakaa usiku ule kambini. 22 Akaondoka usiku ule akawatwaa wakeze wawili, na vijakazi wake wawili, na wanawe kumi na mmoja, akavuka kivuko cha Yaboki. 23 Akawatwaa, akawavusha mto, akavusha na vyote alivyokuwa navyo. 24 Yakobo akakaa peke yake; na mtu mmoja akashindana naye mweleka hata alfajiri. 25 Naye alipoona ya kuwa hamshindi, alimgusa panapo uvungu wa paja lake; ukateguka uvungu wa paja la Yakobo alipokuwa akishindana naye. 26 Akasema, Niache, niende, maana kunapambazuka. Akasema, Sikuachi, usiponibariki. 27 Akamwuliza, Jina lako n'nani? Akasema, Yakobo. 28 Akamwambia, Jina lako hutaitwa tena Yakobo, ila Israeli, maana umeshindana na Mungu, na watu, nawe umeshinda. 29 Yakobo akamwuliza, akasema, Niambie, tafadhali, jina lako? Akasema, Kwa nini waniuliza jina langu? Akambariki huko. 30 Yakobo akapaita mahali pale, Penueli, maana alisema, Nimeonana na Mungu uso kwa uso, na nafsi yangu imeokoka. 31 Jua likamzukia akivuka Penueli, akachechemea kwa sababu ya paja la mguu wake. 32 Kwa hiyo wana wa Israeli hawali ule mshipa ulio katika uvungu wa paja hata leo; maana alimgusa Yakobo panapo uvungu wa paja katika mshipa wa kiuno.

Mwanzo 33

1 Yakobo akainua macho yake, akaona, na tazama, Esau anakuja na watu mia nne pamoja naye. Akawagawanyia Lea, na Raheli, na wale vijakazi wawili, wana wao. 2 Akawaweka hao vijakazi na wana wao mbele, na Lea na wanawe nyuma yao, na Raheli na Yusufu mwisho. 3 Akapita mwenyewe mbele yao, akainama mpaka nchi mara saba, hata alipomkaribia ndugu yake. 4 Esau akaja mbio kumlaki, akamkumbatia, na kumwangukia shingoni, akambusu; nao wakalia. 5 Akainua macho yake, akawaona wale wanawake na watoto, akauliza, Ni nani hawa walio pamoja nawe? Akasema, Ni watoto Mungu aliompa mtumwa wako kwa neema yake. 6 Ndipo wale vijakazi, na wana wao, wakakaribia wakainama. 7 Lea naye, na wanawe, wakakaribia wakainama. Baadaye Yusufu na Raheli wakakaribia, wakainama. 8 Akasema, Kundi hili lote nililolikuta, maana yake ni nini? Akasema, Kunipatia kibali machoni pa bwana wangu. 9 Esau akasema, Ninayo tele, ndugu yangu, uliyo nayo na yawe yako. 10 Yakobo akasema, Sivyo; kama nimekubalika machoni pako tafadhali upokee zawadi yangu mkononi mwangu, iwapo nimeona uso wako kama kuona uso wa Mungu, ukapendezwa nami. 11 Pokea, tafadhali, mbaraka wangu, ulioletewa, kwa sababu Mungu amenineemesha, na kwa sababu ninavyo hivi vyote Akamshurutisha, naye akapokea. 12 Kisha Esau akamwambia, Twende zetu, tusafiri, nami nitakutangulia. 13 Akamjibu, Bwana wangu anajua ya kuwa watoto ni wachanga, tena kondoo na ng'ombe nilio nao wanyonyesha. Hao wanyama wakiharakishwa siku moja, watakufa wote. 14 Tafadhali bwana wangu na apite mbele ya mtumwa wake; nami nitawaongoza polepole kwa kadiri ya mwendo wa wanyama walio mbele yangu, na kwa kadiri ya mwendo wa watoto, hata nitakapofika kwa bwana wangu huko Seiri. 15 Esau akasema, Nikuachie, basi, baadhi ya watu walio pamoja nami. Akasema, Pana haja gani? Na nione kibali tu machoni pa bwana wangu. 16 Basi Esau akarudi siku ile ile akishika njia yake mpaka Seiri. 17 Yakobo akaendelea mpaka Sukothi. Akajijengea nyumba, akawafanyia makundi yake vibanda. Kwa hiyo jina la mahali pale pakaitwa Sukothi. 18 Yakobo akaja kwa amani mpaka mji wa Shekemu, ulio katika nchi ya Kanaani, alipokuja kutoka Padan-aramu; akapiga kambi mbele ya huo mji. 19 Akainunua sehemu ya nchi, alipopiga hema yake, kwa mkono wa wana wa Hamori, baba wa Shekemu, kwa vipande mia vya fedha. 20 Akajenga huko madhabahu, akaiita, El-elohe-Israeli.

Mwanzo 34

1 Basi Dina, binti Lea, ambaye Lea alimzalia Yakobo, akatoka kuwaona binti za nchi. 2 Shekemu, mwana wa Hamori, Mhivi, mkuu wa nchi, akamwona akamtwaa, akalala naye, akambikiri. 3 Moyo wake ukaambatana na Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana, akasema na huyu msichana kwa maneno mazuri. 4 Shekemu akamwambia Hamori, babaye, akasema, Unipatie msichana huyu awe mke wangu. 5 Basi Yakobo akasikia ya kwamba amembikiri Dina, binti yake. Na wanawe walikuwako pamoja na wanyama wake nyikani. Yakobo akanyamaza, hata walipokuja. 6 Akatoka Hamori, babaye Shekemu, kumwendea Yakobo, aseme naye. 7 Wanawe Yakobo waliposikia hayo, wakaja kutoka nyikani; nao wakasikitika sana, wakakasirika mno, kwa sababu amefanya upumbavu katika Israeli kwa kulala na binti Yakobo, neno lisilojuzu kutendeka. 8 Hamori akasema nao, akinena, Roho ya Shekemu, mwanangu, inamtamani binti yenu, tafadhalini, mpeni amwoe. 9 Mkaoane na sisi, mtupe sisi binti zenu, nanyi mkatwae binti zetu. 10 Nanyi mtakaa nasi, na nchi hii itakuwa mbele yenu; kaeni, na kufanya biashara humo, mkapate mali humo. 11 Shekemu akamwambia babaye yule msichana na nduguze, Na nikubalike machoni penu, na mtakavyoniambia nitatoa. 12 Mjapoongeza sana mahari na zawadi, nitatoa kadiri ya mtakavyoniambia, lakini mnipe huyu msichana, awe mke wangu. 13 Wana wa Yakobo wakawajibu Shekemu na Hamori babaye, kwa hila, maana amemharibu Dina, umbu lao, 14 wakawaambia, Hatuwezi kufanya neno hili, tumpe umbu letu mtu asiyetahiriwa; ingekuwa aibu kwetu. 15 Lakini kwa sharti hii tu tutapatana nanyi; mkiwa kama sisi, akitahiriwa kila mwanamume wenu, 16 ndipo tutawapa ninyi binti yetu, na sisi tutatwaa binti zenu tutakaa pamoja nanyi, nasi tutakuwa watu wamoja. 17 Lakini kama hamtusikii na kutahiriwa, basi tutamtwaa umbu letu, nasi tutakwenda zetu. 18 Maneno yao yakawa mema machoni pa Hamori, na machoni pa Shekemu, mwana wa Hamori. 19 Na yule kijana hakukawia kulifanya neno lile, maana amependezewa na binti Yakobo, naye alikuwa mwenye heshima kuliko wote nyumbani mwa babaye. 20 Hamori, na Shekemu mwanawe, wakaja langoni pa mji wao, wakasema na watu wa mji wao, wakinena, 21 Watu hawa wana amani nasi, basi na wakae katika nchi, na kufanya biashara humo; kwa maana nchi ni kubwa, yawatosha; na tuwatwae binti zao kuwa wake zetu, na binti zetu tuwape wao. 22 Lakini kwa sharti hiyo moja tu watapatana nasi wakae wote kwetu, tuwe watu wamoja, kama tukitahiriwa kila mwanamume, kama hawa walivyotahiriwa. 23 Je! Kondoo zao, na mali zao, na wanyama wao wote hawatakuwa mali zetu? Basi na tupatane nao tu, nao watakaa kwetu. 24 Wakawasikia Hamori na Shekemu mwanawe, wote watokao katika lango la mji wake. Wakatahiriwa kila mwanamume, wote watokao katika lango la mji wake. 25 Ikawa siku ya tatu, walipokuwa wakiumwa sana, wana wawili wa Yakobo, Simeoni na Lawi, nduguze Dina, wakatwaa kila mtu upanga wake, wakaujia mji kwa ujasiri, wakawaua waume wote. 26 Wakawaua Hamori, na Shekemu mwanawe, kwa makali ya upanga, wakamtwaa Dina katika nyumba ya Shekemu, wakatoka. 27 Wana wa Yakobo wakawajilia hao waliouawa, wakauteka nyara mji kwa sababu wamemharibu umbu lao. 28 Wakachukua kondoo zao, na ng'ombe zao, na punda zao, na vitu vilivyokuwamo mjini, navyo vilivyokuwako kondeni. 29 Wakatwaa na mali zao zote, na watoto wao wote, na wake zao, na vyote vilivyokuwamo nyumbani mwao wakavichukua mateka. 30 Yakobo akawaambia Simeoni na Lawi, Mmenitaabisha, kunifanya ninuke vibaya kati ya watu wa nchi hii, Wakanaani na Waperizi; na mimi, kwa kuwa watu wangu ni haba, watanikusanyikia, na kunipiga, nami nitaangamizwa, mimi na nyumba yangu. 31 Nao wakasema, Je! Ni vema amtendee umbu letu kama kahaba?

Mwanzo 35

1 Mungu akamwambia Yakobo, Ondoka, panda uende Betheli, ukakae huko; ukamfanyie Mungu madhabahu huko; yeye aliyekutokea ulipomkimbia Esau, ndugu yako. 2 Yakobo akawaambia watu wa nyumbani mwake, na wote waliokuwa pamoja naye, Ondoeni miungu migeni iliyoko kwenu, mjisafishe mkabadili nguo zenu. 3 Tuondoke, tupande kwenda Betheli, nami nitamfanyia Mungu madhabahu huko; yeye aliyenisikia siku ya shida yangu, akawa pamoja nami katika njia yote niliyoiendea. 4 Nao wakampa Yakobo miungu migeni yote iliyokuwa mikononi mwao, na pete zilizokuwa masikioni mwao, naye Yakobo akazificha chini ya mwaloni ulioko Shekemu. 5 Wakashika njia, hofu ya Mungu ikaishika miji iliyowazunguka, wala hawakuwafuata wana wa Yakobo. 6 Basi Yakobo akafika Luzu, ulio katika nchi ya Kanaani, ndio Betheli, yeye na watu wote waliokuwa pamoja naye. 7 Akajenga huko madhabahu, akapaita mahali pale, El-Betheli; kwa sababu huko Mungu alimtokea, hapo alipomkimbia ndugu yake. 8 Akafa Debora mlezi wa Rebeka, akazikwa chini ya Betheli, chini ya mwaloni; na jina lake likaitwa Alon-bakuthi. 9 Mungu akamtokea Yakobo tena, aliporudi kutoka Padan-aramu akambariki. 10 Mungu akamwambia, Jina lako ni Yakobo; hutaitwa tena Yakobo, lakini Israeli litakuwa jina lako. Akamwita jina lake, Israeli. 11 Mungu akamwambia, Mimi ni Mungu Mwenyezi, uzidi ukaongezeke. Taifa na kundi la mataifa watatoka kwako, na wafalme watatoka viunoni mwako. 12 Na nchi hii niliyowapa Ibrahimu na Isaka nitakupa wewe, na uzao wako baada yako nitawapa nchi hiyo. 13 Mungu akakwea juu kutoka kwake mahali hapo aliposema naye. 14 Yakobo akasimamisha nguzo mahali aliposema naye, nguzo ya mawe, akamimina juu yake sadaka ya kinywaji, akamimina mafuta juu yake. 15 Yakobo akapaita mahali pale, Mungu aliposema naye, Betheli. 16 Wakasafiri kutoka Betheli, hata ukabaki mwendo wa kitambo tu kufika Efrathi, Raheli akashikwa na utungu wa kuzaa, na utungu wake ulikuwa mzito. 17 Ikawa alipokuwa anashikwa sana na utungu, mzalisha akamwambia, Usiogope, maana sasa utamzaa mwanamume mwingine. 18 Ikawa hapo katika kutoa roho yake, maana alikufa, akamwita jina lake Benoni, lakini babaye alimwita Benyamini. 19 Akafa Raheli, akazikwa katika njia ya Efrathi, ndio Bethlehemu. 20 Yakobo akasimamisha nguzo juu ya kaburi lake, ndiyo nguzo ya kaburi la Raheli hata leo. 21 Kisha akasafiri Israeli akapiga hema yake upande wa pili wa mnara wa Ederi. 22 Ikawa Israeli alipokuwa akikaa katika nchi ile, Reubeni akaenda akalala na Bilha, suria wa babaye; Israeli akasikia habari. Basi hao wana wa Yakobo walikuwa kumi na wawili. 23 Wana wa Lea ni Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, na Simeoni, na Lawi, na Yuda, na Isakari, na Zabuloni. 24 Wana wa Raheli, ni Yusufu na Benyamini. 25 Wana wa Bilha, kijakazi wa Raheli, ni Dani na Naftali. 26 Wana wa Zilpa, kijakazi wa Lea, ni Gadi na Asheri. Hawa ndio wana wa Yakobo aliozaliwa katika Padan-aramu. 27 Yakobo akaja kwa Isaka, babaye, huko Mamre, mji wa Arba, ndio Hebroni, walipokaa ugenini Ibrahimu na Isaka. 28 Siku za Isaka zilikuwa miaka mia na themanini. 29 Naye Isaka akakata roho, akafa, akakusanyika kwa watu wake, ni mzee, ameshiba siku. Esau na Yakobo, wanawe, wakamzika

Mwanzo 36

1 Hivi ndivyo vizazi vya Esau, ndiye Edomu. 2 Esau alitwaa binti za Kanaani, kuwa wakeze; Ada, binti Eloni, Mhiti, na Oholibama, binti Ana, binti Sibeoni, Mhivi; 3 na Basemathi, binti Ishmaeli, nduguye Nebayothi. 4 Ada akamzalia Esau Elifazi; na Basemathi alizaa Reueli. 5 Oholibama alizaa Yeushi, na Yalamu, na Kora. Hao ndio wana wa Esau aliozaliwa katika nchi ya Kanaani. 6 Esau akawatwaa wakeze, na wanawe, na binti zake, na watu wote wa nyumbani mwake, na ng'ombe zake, na wanyama wake wote, na mali yake yote, aliyoyapata katika nchi ya Kanaani; akaenda mpaka nchi iliyo mbali na Yakobo nduguye. 7 Maana mali yao yalikuwa mengi wasiweze kukaa pamoja, wala haikuweza nchi ya kusafiri kwao kuwachukua, kwa sababu ya wanyama wao. 8 Esau akakaa katika mlima Seiri, Esau ndiye Edomu. 9 Hivi ni vizazi vya Esau, baba ya Edomu katika mlima Seiri. 10 Haya ndiyo majina ya wana wa Esau; Elifazi, mwana wa Ada mkewe Esau. Reuli, mwana wa Basemathi, mkewe Esau. 11 Na wana wa Elifazi, ni Temani na Omari, na Sefo, na Gatamu, na Kenazi. 12 Na Timna alikuwa suria wa Elifazi, mwana wa Esau; naye akamzalia Elifazi Amaleki. Hao ndio wana wa Ada, mkewe Esau. 13 Na hawa ni wana wa Reueli, Nahathi, na Zera, na Shama na Miza. Hao walikuwa wana wa Basemathi, mkewe Esau. 14 Na hawa ni wana wa Oholibama, binti Ana, binti Sibeoni, mkewe Esau; akamzalia Esau, Yeushi, na Yalamu, na Kora. 15 Hawa ndio majumbe wao wana wa Esau; wana wa Elifazi, mzaliwa wa kwanza wa Esau; jumbe Temani, jumbe Omari, jumbe Sefo, jumbe Kenazi, 16 jumbe Kora, jumbe Gatamu, jumbe Amaleki. Hao ndio majumbe, waliotoka kwa Elifazi katika nchi ya Edomu. Hao ni wana wa Ada. 17 Na hawa ni wana wa Reueli, mwanawe Esau; jumbe Nahathi, jumbe Zera, jumbe Shama, jumbe Miza. Hao ndio majumbe waliotoka kwa Reueli katika nchi ya Edomu. Hao ni wana wa Basemathi, mkewe Esau. 18 Na hawa ni wana wa Oholibama, mkewe Esau; jumbe Yeushi, jumbe Yalamu, jumbe Kora. Hao ndio majumbe waliotoka kwa Oholibama, binti Ana, mkewe Esau. 19 Hao ni wana wa Esau, na hao ndio majumbe wao; naye Esau ndiye Edomu. 20 Hawa ni wana wa Seiri, Mhori, wenyeji wa nchi ile; Lotani, na Shobali, na Sibeoni, na Ana, 21 na Dishoni, na Eseri, na Dishani. Hao ndio majumbe waliotoka katika Wahori, wana wa Seiri, katika nchi ya Edomu. 22 Na wana wa Lotani, ni Hori, na Hemamu; na umbu lake Lotani ni Timna. 23 Na hawa ni wana wa Shobali, Alvani, na Manahathi, na Ebali, na Shefo, na Onamu. 24 Na hawa ni wana wa Sibeoni, Aya, na Ana; ni yule Ana aliyeona chemchemi za maji ya moto katika jangwa, alipokuwa akichunga punda za Sibeoni babaye. 25 Na hawa ni wana wa Ana, Dishoni, na Oholibama, binti Ana. 26 Na hawa ni wana wa Dishoni, Hemdani, na Eshbani, na Ithrani, na Kerani. 27 Na hawa ni wana wa Eseri, Bilhani, na Zaawani, na Akani. 28 Na hawa ni wana wa Dishani, Usi, na Arani. 29 Hawa ndio majumbe waliotoka katika Wahori; jumbe Lotani, jumbe Shobali, jumbe Sibeoni, jumbe Ana, 30 jumbe Dishoni, jumbe Eseri jumbe Dishani. Hao ndio majumbe waliotoka katika Wahori, kwa habari za majumbe yao, katika nchi ya Seiri. 31 Na hawa ndio wafalme waliomiliki katika nchi ya Edomu, kabla ya kumiliki mfalme ye yote juu ya wana wa Israeli. 32 Bela wa Beori alimiliki katika Edomu, na jina la mji wake ni Dinhaba. 33 Akafa Bela, akamiliki Yobabu mwana wa Zera, wa Bosra, badala yake. 34 Akafa Yobabu, akamiliki Hushamu, wa nchi ya Watemani, badala yake. 35 Akafa Hushamu, akamiliki Hadadi wa Bedadi badala yake, naye ndiye aliyepiga Midiani katika nyika ya Moabu, na jina la mji wake ni Avithi. 36 Akafa Hadadi, akamiliki Samla wa Masreka badala yake. 37 Akafa Samla, na Shauli wa Rehobothi, ulio karibu na mto, akamiliki badala yake. 38 Akafa Shauli, akamiliki Baal-hanani, mwana wa Akbori, badala yake. 39 Akafa Baal-hanani, mwana wa Akbori, akamiliki Hadadi badala yake; na jina la mji wake ni Pau; na jina la mkewe ni Mehetabeli, binti Matredi, binti Mezahabu. 40 Na hayo ndiyo majina ya majumbe waliotoka kwa Esau, kufuata jamaa zao, na mahali pao, kwa majina yao. Jumbe Timna, jumbe Alva, jumbe Yethethi, 41 jumbe Oholibama, jumbe Ela, jumbe Pinoni, 42 jumbe Kenazi, jumbe Temani, jumbe Mibsari, 43 jumbe Magdieli, jumbe Iramu. Hao ndio majumbe wa Edomu, kufuata makao yao, katika nchi ya mamlaka yao. Naye huyo ndiye Esau, baba ya Edomu.

Mwanzo 37

1 Yakobo akakaa katika nchi aliyosafiri baba yake, katika nchi ya Kanaani. 2 Hivi ndivyo vizazi vya Yakobo. Yusufu, aliyekuwa mwenye miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake; naye alikuwa kijana pamoja na wana wa Bilha, na wana wa Zilpa, wake wa baba yake. Yusufu akamletea baba yao habari zao mbaya. 3 Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. 4 Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. 5 Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; 6 akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. 7 Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. 8 Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. 9 Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. 10 Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? 11 Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili. 12 Ndugu zake wakaenda kuchunga kondoo za baba yao huko Shekemu. 13 Israeli akamwambia Yusufu, Je! Ndugu zako hawachungi kondoo katika Shekemu? Njoo, nikutume kwao. Akamwambia, Mimi hapa. 14 Akamwambia, Enenda, basi, ukaone kama ndugu zako hawajambo, na kundi nalo li salama, ukaniletee habari. Basi akampeleka kutoka bonde la Hebroni, akafika Shekemu. 15 Mtu mmoja akamkuta, naye alikuwa anazunguka-zunguka katika nyika; yule mtu akamwuliza, akisema, Unatafuta nini? 16 Akasema, Nawatafuta ndugu zangu; tafadhali uniambie mahali wanakochunga. 17 Yule mtu akasema, Wametoka hapa, maana niliwasikia wakisema, Twendeni Dothani. Basi Yusufu akawafuata ndugu zake akawakuta huko Dothani. 18 Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. 19 Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. 20 Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. 21 Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. 22 Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika hii iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. 23 Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, 24 wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji. 25 Nao wakakaa kitako kula chakula; wakainua macho yao, wakaona, msafara wa Waishmaeli wanakuja wakitoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri. 26 Yuda akawaambia ndugu zake, Kwafaa nini kumwua ndugu yetu, na kuificha damu yake? 27 Haya, na tumwuze kwa hawa Waishmaeli, wala mikono yetu isimdhuru, maana yeye ni ndugu yetu, na damu yetu. Ndugu zake wakakubali. 28 Wakapita wafanya biashara Wamidiani; basi wakamtoa Yusufu, wakampandisha kumtoa katika birika, wakamwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande vya fedha ishirini; nao wakamchukua Yusufu mpaka Misri. 29 Akarudi Reubeni birikani, kumbe! Yusufu hayumo katika birika, akararua nguo zake. 30 Akarudi kwa ndugu zake, akasema, Mtoto hayuko, nami niende wapi? 31 Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. 32 Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. 33 Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. 34 Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi. 35 Wanawe wote, na binti zake wote, wakaondoka wamtulize, lakini akakataa kutulizwa, akasema, La! Nitamshukia mwanangu, nikisikitika, hata kuzimu. Baba yake akamlilia. 36 Nao Wamidiani wakamwuza huko Misri, kwa Potifa, akida wa Farao, mkuu wa askari.

Mwanzo 38

1 Ikawa wakati ule, Yuda akashuka kutoka kwa ndugu zake, akamfikia mtu Mwadulami, jina lake Hira. 2 Yuda akaona huko binti wa mtu Mkanaani, jina lake Shua. Akamtwaa, akaingia kwake. 3 Naye akapata mimba, akazaa mwana, akamwita jina lake Eri. 4 Akapata mimba tena, akazaa mwana, akamwita jina lake Onani. 5 Akaendelea, akazaa tena mwana mwingine, akamwita jina lake Shela. Naye Yuda alikuwako huko Kezibu, alipomzaa. 6 Yuda akamwoza mke Eri, mzaliwa wake wa kwanza, na jina lake huyo mke ni Tamari. 7 Naye Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mbaya machoni pa Bwana; na Bwana akamwua. 8 Yuda akamwambia Onani, Uingie kwa mke wa nduguyo, ukamwoe, ukamwinulie nduguyo uzao. 9 Onani alijua ya kwamba huo uzao hautakuwa wake, ikawa, alipoingia kwa mke wa nduguye, akamwagia chini asimpe nduguye uzao. 10 Neno hili alilolifanya likawa baya machoni pa Bwana, basi akamwua yeye naye. 11 Yuda akamwambia Tamari mkwewe, Ukae mjane nyumbani mwa baba yako hata Shela mwanangu atakapokuwa mtu mzima, maana alisema, Asipate kufa yeye kama nduguze. Basi Tamari akaenda, akakaa nyumbani mwa babaye. 12 Siku nyingi zikapita, akafa binti Shua, mkewe Yuda. Yuda akafarijika, akaenda kwa watu wake wawakatao manyoya kondoo huko Timna, yeye na mwenzake Hira, Mwadulami. 13 Huyo Tamari akapewa habari, kusema, Mkweo anakwenda Timna, akate manyoya ya kondoo zake. 14 Basi akavua nguo za ujane wake, akajivika utaji, akajifunika uso, akakaa mlangoni pa Enaimu, karibu na njia ya kuendea Timna. Maana aliona ya kwamba Shela amekuwa mtu mzima, wala hakuozwa awe mkewe. 15 Yuda alipomwona alimdhania kuwa ni kahaba, maana amejifunika uso. 16 Akamgeukia kando ya njia, akasema, Niruhusu niingie kwako. Maana hakujua ya kuwa ni mkwewe. Akamwuliza, Utanipa nini, ukiingia kwangu? 17 Akasema, Nitakuletea mwana-mbuzi wa kundini. Naye akamwuliza, Je! Utanipa rehani hata utakapomleta? 18 Akasema, Nikupe rehani gani? Akamjibu, Pete yako ya muhuri, na kamba yake, na fimbo yako iliyo mkononi mwako. Basi akampa, akaingia kwake, naye akapata mimba. 19 Akaondoka, akaenda zake, akavua utaji wake, na kuvaa mavazi ya ujane wake. 20 Yuda akapeleka yule mwana-mbuzi kwa mkono wa rafiki yake Mwadulami, ili aipate rehani mkononi mwa huyo mwanamke lakini hakumkuta. 21 Akauliza watu wa mahali pale, akisema, Yuko wapi yule kahaba aliyekuwapo Enaimu kando ya njia? Wakasema, Hakuwako hapa kahaba. 22 Akamrudia Yuda akasema, Sikumwona; hata na watu wa mahali hapo walisema, Hakuwako kahaba. 23 Yuda akasema, Na aichukue yeye, tusije tukatiwa aibu; tazama, nimempelekea mbuzi huyu, wala hukumkuta. 24 Ikawa baada ya miezi mitatu Yuda akapewa habari kwamba, Mkweo, Tamari, amefanya uzinifu, naye ana mimba ya haramu. Yuda akasema, Mtoeni ateketezwe. 25 Alipotolewa, alipeleka watu kwa mkwewe, akisema, Mimi nimepewa mimba na mtu mwenye vitu hivi. Akasema, Tambua basi, vitu hivi ni vya nani, pete hii, na kamba hii, na fimbo hii. 26 Yuda akavikiri, akasema, Yeye ni mwenye haki kuliko mimi, kwa kuwa sikumpa Shela, mwanangu. Wala hakumjua tena baada ya hayo. 27 Ikawa, wakati wake wa kuzaa walikuwapo mapacha tumboni mwake. 28 Ikawa alipokuwa akizaa, mtoto mmoja akatoa mkono, mzalisha akautwaa uzi mwekundu akaufunga mkononi mwake, huku akisema, Huyu ametoka kwanza. 29 Ikawa aliporudisha mkono wake, tazama, ndugu yake akatoka. Akasema, Mbona umepita kwa nguvu wewe? Mambo ya nguvu na yakuandame. Kwa hiyo jina lake likaitwa Peresi. 30 Akatoka ndugu yake baadaye, ana uzi mwekundu mkononi mwake; naye akaitwa jina lake Zera.

Mwanzo 39

1 Basi Yusufu akaletwa mpaka Misri naye Potifa, akida wa Farao, mkuu wa askari, mtu wa Misri, akamnunua mkononi mwa hao Waishmaeli waliomleta huko. 2 Bwana akawa pamoja na Yusufu, naye akasitawi; naye alikuwa katika nyumba ya bwana wake, yule Mmisri. 3 Bwana wake akaona ya kwamba Bwana yu pamoja naye, na ya kuwa Bwana anafanikisha mambo yote mkononi mwake. 4 Yusufu akaona neema machoni pake, akamtumikia. Naye akamweka awe msimamizi juu ya nyumba yake, na yote yaliyomo akayaweka mkononi mwake. 5 Ikawa tokea wakati alipomweka awe msimamizi juu ya nyumba yake, na vyote vilivyomo, Bwana akabariki nyumba ya yule Mmisri kwa ajili ya Yusufu. Mbaraka wa Bwana ukawa juu ya vyote alivyokuwa navyo katika nyumba, na katika shamba. 6 Akayaacha yote aliyokuwa nayo mkononi mwa Yusufu; wala hakujua habari za kitu cho chote chake, ila hicho chakula alichokula tu. 7 Ikawa baada ya mambo hayo, mke wa bwana wake akamtamani Yusufu, akamwambia, Lala nami. 8 Lakini akakataa, akamwambia mke wa bwana wake, Tazama, bwana wangu hajui kitu kilichowekwa kwangu nyumbani, na vyote alivyo navyo amevitia mkononi mwangu. 9 Hakuna mkuu katika nyumba hii kuliko mimi, wala hakunizuilia kitu cho chote ila wewe, kwa kuwa wewe u mkewe. Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu? 10 Akawa akizidi kusema na Yusufu siku baada ya siku, lakini hakumsikia alale naye, wala aongee naye. 11 Ikawa, siku moja, akaingia nyumbani atende kazi yake, wala hapakuwa na mtu katika watu wa nyumbani humo ndani; 12 huyo mwanamke akamshika nguo zake, akisema, Lala nami. Yusufu akaiacha nguo yake mkononi mwake, akakimbia, akatoka nje. 13 Ikawa alipoona ya kwamba amemwachilia nguo yake mkononi mwake, naye amekimbia nje, 14 akawaita watu wa nyumbani mwake, akasema nao, akinena, Angalieni, ametuletea mtu Mwebrania atufanyie dhihaka. Ameingia kwangu, ili alale nami, nikalia kwa sauti kuu. 15 Ikawa, aliposikia ya kuwa nimepaza sauti yangu na kulia, aliiacha nguo yake kwangu, akakimbia, akatoka nje. 16 Basi akaiweka ile nguo kwake hata bwana wake aje nyumbani. 17 Naye akamwambia kama maneno hayo, akisema, Yule mtumwa Mwebrania uliyemleta kwetu, aliingia kwangu anidhihaki. 18 Ikawa nilipopaza sauti yangu, nikalia, akaacha nguo yake kwangu akakimbia nje. 19 Ikawa bwana wake aliposikia maneno ya mkewe aliyomwambia, akisema, Mtumwa wako amenitendea mambo kama haya, hasira yake ikawaka. 20 Bwana wake akamtwaa Yusufu, akamtia gerezani, mahali walipofungwa wafungwa wa mfalme, naye akawamo humo gerezani. 21 Lakini Bwana akawa pamoja na Yusufu, akamfadhili, akampa kibali machoni pa mkuu wa gereza. 22 Mkuu wa gereza akawatia mkononi mwa Yusufu watu wote waliofungwa, waliomo gerezani; na yote yaliyofanyika humo ndiye aliyeyafanya. 23 Wala mkuu wa gereza hakuangalia neno lililoko mkononi mwa Yusufu; kwa kuwa Bwana alikuwa pamoja naye. Bwana akayafanikisha yote aliyoyafanya.

Mwanzo 40

1 Ikawa, baada ya mambo hayo, mnyweshaji wa mfalme wa Misri, na mwokaji wake, wakamkosa bwana wao, mfalme wa Misri. 2 Farao akawaghadhibikia maakida wake wawili, mkuu wa wanyweshaji na mkuu wa waokaji. 3 Akawatia katika lindo nyumbani mwa mkuu wa askari, humo gerezani, mahali alipofungwa Yusufu. 4 Mkuu wa askari akamwekea Yusufu watu hao, naye akawahudumu, nao wakakaa siku kadha wa kadha katika kifungo. 5 Wakaota ndoto wote wawili, kila mtu ndoto yake usiku mmoja, kila mtu kwa tafsiri ya ndoto yake, mnyweshaji na mwokaji wa mfalme wa Misri waliofungwa gerezani. 6 Yusufu akawajia asubuhi, akawaona wamefadhaika. 7 Akawauliza hao maakida wa Farao, waliokuwa pamoja naye katika kifungo, nyumbani mwa bwana wake, akisema, Mbona nyuso zenu zimekunjamana leo? 8 Wakamwambia, Tumeota ndoto wala hapana awezaye kuifasiri. Yusufu akawaambia, Kufasiri si kazi ya Mungu? Tafadhalini mniambie. 9 Mnyweshaji mkuu akamhadithia Yusufu ndoto yake; akamwambia, Katika ndoto yangu nimeota, uko mzabibu mbele yangu. 10 Na katika mzabibu mlikuwa na matawi matatu, nao ulikuwa kana unamea, unachanua maua, vishada vyake vikatoa zabibu zilizoiva. 11 Na kikombe cha Farao kilikuwa mkononi mwangu, nikazitwaa zabibu, nikazikamua katika kikombe cha Farao, nikampa Farao kikombe mkononi mwake. 12 Yusufu akamwambia, Tafsiri yake ndiyo hii. Matawi matatu ni siku tatu. 13 Baada ya siku tatu Farao atakiinua kichwa chako, atakurudisha katika kazi yako; nawe utampa Farao kikombe mkononi mwake, kama desturi ya kwanza, ulipokuwa mnyweshaji wake. 14 Ila unikumbuke mimi, utakapopata mema, ukanifanyie fadhili, nakuomba, ukanitaje kwa Farao, na kunitoa katika nyumba hii. 15 Kwa sababu hakika naliibiwa kutoka nchi ya Waebrania, wala hapa sikutenda neno lo lote hata wanitie gerezani. 16 Mkuu wa waokaji alipoona ya kwamba hiyo tafsiri ni ya mema, akamwambia Yusufu, Mimi kadhalika nilikuwa katika ndoto yangu, na tazama, ziko nyungo tatu za mikate myeupe juu ya kichwa changu. 17 Na katika ungo wa juu, mlikuwa na kila namna ya chakula kwa Farao, kazi za mwokaji; ndege wakavila katika ungo juu ya kichwa changu. 18 Yusufu akajibu, akasema, Tafsiri yake ndiyo hii Nyungo tatu ni siku tatu. 19 Baada ya siku tatu Farao atakiinua na kukuondolea kichwa chako, na kukutundika juu ya mti, na ndege watakula nyama yako. 20 Ikawa siku ya tatu, siku ya kuzaliwa kwake Farao, akawafanyia karamu watumwa wake wote; akakiinua kichwa cha mkuu wa wanyweshaji, na cha mkuu wa waokaji, miongoni mwa watumwa wake. 21 Akamrudisha mkuu wa wanyweshaji katika kazi yake ya kunywesha, naye akampa Farao kikombe mkononi mwake. 22 Bali akamtundika mkuu wa waokaji, kama Yusufu alivyowafasiria. 23 Lakini huyo mkuu wa wanyweshaji hakumkumbuka Yusufu, alimsahau.

Mwanzo 41

1 Ikawa, mwisho wa miaka miwili mizima, Farao akaota ndoto; na tazama, amesimama kando ya mto. 2 Na tazama, ng'ombe saba wazuri, wanono, walipanda kutoka mtoni, wakajilisha manyasini. 3 Na tazama, ng'ombe saba wengine wakapanda nyuma yao kutoka mtoni, wabaya, wamekonda, wakasimama karibu na wale ng'ombe wengine ukingoni mwa mto. 4 Kisha hao ng'ombe wabaya waliokonda wakawala wale ng'ombe saba wazuri, wanono. Basi Farao akaamka. 5 Akalala, akaota ndoto mara ya pili. Tazama, masuke saba yalimea katika bua moja, makubwa, mema. 6 Na tazama, masuke saba membamba, yamekaushwa na upepo wa mashariki, yakatokeza baada yao. 7 Kisha hayo masuke membamba saba yakayala yale masuke saba makubwa yaliyojaa. Basi Farao akaamka, kumbe! Ni ndoto tu. 8 Hata asubuhi roho yake ikafadhaika; akapeleka watu kuwaita waganga wote wa Misri, na watu wote wenye hekima walioko. Farao akawahadithia ndoto yake, wala hakuna aliyeweza kumfasiria Farao mambo hayo. 9 Basi mkuu wa wanyweshaji akamwambia Farao akisema, Nayakumbuka makosa yangu leo. 10 Farao aliwakasirikia watumwa wake, akanitia nifungwe nyumbani mwa mkuu wa askari, mimi na mkuu wa waokaji. 11 Tukaota ndoto usiku mmoja, mimi na yeye; kila mtu kwa tafsiri ya ndoto yake tukaota. 12 Na huko pamoja nasi palikuwa na kijana; Mwebrania, mtumishi wa mkuu wa askari, tukamhadithia, naye akatufasiria ndoto zetu; akamfasiria kila mtu kama ilivyokuwa ndoto yake. 13 Ikawa, kama vile alivyotufasiria ndivyo ilivyotokea; mimi nalirudishwa katika kazi yangu, na yeye alitundikwa. 14 Ndipo Farao akapeleka watu, akamwita Yusufu, wakamleta upesi kutoka gerezani. Akanyoa, akabadili nguo zake, na kuingia kwa Farao. 15 Farao akamwambia Yusufu, Nimeota ndoto, wala hakuna awezaye kunifasiria; nami nimesikia habari zako, ya kwamba, usikiapo ndoto, waweza kuifasiri. 16 Yusufu akamjibu Farao, akisema, Si mimi; Mungu atampa Farao majibu ya amani. 17 Farao akamwambia Yusufu, Katika ndoto yangu nalikuwa nikisimama ukingoni mwa mto; 18 na tazama, ng'ombe saba wanatoka mtoni, wanono, wazuri, wakajilisha manyasini. 19 Kisha, tazama, ng'ombe saba wengine wakapanda baada yao, dhaifu, wabaya sana, wamekonda; katika nchi yote ya Misri sijaona kama hao kwa udhaifu. 20 Na hao ng'ombe waliokonda, wabaya, wakawala wale ng'ombe saba wa kwanza, wale wanono. 21 Na walipokwisha kuwala haikutambulikana ya kwamba wamewala, bali wakaonekana wabaya kama kwanza. Basi nikaamka. 22 Kisha nikaona katika ndoto yangu, na tazama, masuke saba yanatokeza katika bua moja, mema, yamejaa. 23 Na tazama, masuke saba membamba, dhaifu, yamekaushwa na upepo wa mashariki, yakatokeza baada yao. 24 Na hayo masuke dhaifu yakameza yale masuke saba mema. Nami nikawaambia hao waganga, wala hakuna aliyeweza kunionyesha maana yake. 25 Yusufu akamwambia Farao, Ndoto ya Farao ni moja; Mungu amemwonyesha Farao atakayoyafanya hivi karibu. 26 Wale ng'ombe saba wema ni miaka saba; na yale masuke saba mema ni miaka saba. Ndoto ni moja. 27 Na wale ng'ombe saba, dhaifu, wabaya, waliopanda baada yao, ni miaka saba; na yale masuke saba matupu yaliyokaushwa na upepo wa mashariki, yatakuwa miaka saba ya njaa. 28 Ndivyo nilivyomwambia Farao, ya kwamba Mungu amemwonyesha Farao atakayoyafanya hivi karibu. 29 Tazama, miaka saba ya shibe inakuja, katika nchi yote ya Misri. 30 Kisha kutakuja miaka saba ya njaa baada yake; na shibe ile yote itasahauliwa katika nchi ya Misri, na njaa itaiharibu nchi. 31 Wala shibe ile haitajulikana katika nchi kwa sababu ya njaa inayokuja baadaye, maana itakuwa nzito sana. 32 Na ndoto ya Farao kwa vile ilivyokuja mara mbili, ni kwa sababu neno hilo Mungu amelithibitisha, na Mungu atalitimiza upesi. 33 Basi, Farao na ajitafutie mtu wa akili na hekima amweke juu ya nchi ya Misri. 34 Farao na afanye hivi, tena akaweke wasimamizi juu ya nchi, na kutwaa sehemu ya tano katika nchi ya Misri, katika miaka hii saba ya kushiba. 35 Na wakusanye chakula chote cha miaka hii myema ijayo, wakaweke akiba ya nafaka mkononi mwa Farao wakakilinde kuwa chakula katika miji. 36 Na hicho chakula kitakuwa akiba ya nchi kwa ajili ya miaka hiyo saba ya njaa, itakayokuwa katika nchi ya Misri, nchi isiharibike kwa njaa. 37 Neno hilo likawa jema machoni pa Farao, na machoni pa watumwa wake wote. 38 Farao akawaambia watumwa wake, Tupate wapi mtu kama huyu, mwenye roho ya Mungu ndani yake? 39 Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. 40 Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. 41 Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. 42 Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake. 43 Akampandisha katika gari lake la pili alilokuwa nalo. Na watu wakapiga kelele mbele yake, Pigeni magoti. Hivyo akamweka juu ya nchi yote ya Misri. 44 Farao akamwambia Yusufu, Mimi ni Farao, na bila amri yako, mtu asiinue mkono wala mguu katika nchi yote ya Misri. 45 Farao akamwita Yusufu, Safenath-panea; akamwoza Asenathi, binti Potifera, kuhani wa Oni, kuwa mkewe Yusufu akaenda huko na huko katika nchi yote ya Misri. 46 Naye Yusufu alikuwa mwenye miaka thelathini, aliposimama mbele ya Farao, mfalme wa Misri. Yusufu akatoka mbele ya uso wa Farao, akapita katika nchi yote ya Misri. 47 Ikawa katika miaka ile saba ya shibe, nchi ikazaa kwa wingi. 48 Akakusanya chakula chote cha miaka ile saba katika nchi ya Misri. Akaweka chakula katika miji; chakula cha mashamba yaliyouzunguka kila mji, akakiweka ndani yake. 49 Yusufu akakusanya nafaka kama mchanga wa pwani, nyingi mno, hata akaacha kuhesabu, maana ilikuwa haina hesabu. 50 Kabla ya kuja miaka ya njaa, Yusufu akazaliwa wana wawili, ambao Asenathi, binti Potifera, kuhani wa Oni, alimzalia. 51 Yusufu akamwita jina lake yule aliyezaliwa kwanza, Manase, maana alisema, Mungu amenisahaulisha taabu zangu zote, na nyumba yote ya baba yangu. 52 Na wa pili akamwita jina lake Efraimu, maana alisema, Mungu amenipa uzazi katika nchi ya mateso yangu. 53 Miaka ile saba ya shibe ikaisha katika nchi ya Misri, 54 ikaanza kuja miaka ile saba ya njaa, kama vile Yusufu alivyosema. Kukawa na njaa katika nchi zote, bali katika nchi yote ya Misri palikuwa na chakula. 55 Na nchi yote ya Misri ilipoona njaa, watu walimlilia Farao awape chakula. Farao akawaambia Wamisri wote, Enendeni kwa Yusufu; atakavyowaambia, fanyeni. 56 Njaa ikawa katika dunia yote pia. Yusufu akazifungua ghala zote, akawauzia Wamisri. Njaa ikawa nzito katika nchi ya Misri. 57 Watu wa nchi zote wakaja Misri kwa Yusufu; ili wanunue nafaka; kwa sababu njaa imekuwa nzito katika dunia yote.

Mwanzo 42

1 Basi Yakobo akaona ya kuwa kuna nafaka katika Misri, Yakobo akawaambia wanawe, Kwa nini mnatazamana? 2 Akasema, Angalia, nimesikia ya kuwa kuna nafaka Misri; shukeni huko mkatununulie chakula, tupate kuishi wala tusife. 3 Basi ndugu kumi wa Yusufu wakashuka Misri ili wanunue nafaka. 4 Walakini Benyamini, ndugu wa Yusufu, Yakobo hakumpeleka pamoja na ndugu zake, maana alisema, Mabaya yasimpate. 5 Wana wa Israeli wakaja wanunue chakula miongoni mwao waliokuja, kwa kuwa kulikuwa na njaa katika nchi ya Kanaani. 6 Naye Yusufu alikuwa ni liwali juu ya nchi, ndiye aliyewauzia watu wote wa nchi. Nao ndugu zake Yusufu wakaja, wakainama kifudifudi mbele yake. 7 Yusufu akawaona nduguze, akawatambua, lakini alijifanya kama mgeni kwao. Akasema nao kwa maneno makali, akawaambia, Mmetoka wapi ninyi? Wakasema. Tumetoka nchi ya Kanaani, ili tununue chakula. 8 Yusufu akawatambua nduguze, bali wao hawakumtambua yeye. 9 Yusufu akazikumbuka zile ndoto alizowaotea. Akawaambia, Wapelelezi ninyi, mmekuja ili mwuone utupu wa nchi. 10 Wakamwambia, Hasha, bwana, watumwa wako tumekuja ili tununue chakula. 11 Sisi sote ni wana wa mtu mmoja tu watu wa kweli sisi; watumwa wako si wapelelezi. 12 Akawaambia, Sivyo, mmekuja ili mwuone utupu wa nchi. 13 Wakamwambia, Sisi watumwa wako tu ndugu kumi na wawili, wana wa mtu mmoja katika nchi ya Kanaani; na mdogo wetu yuko pamoja na baba yetu leo, na mmoja hayuko. 14 Yusufu akawaambia, Ndivyo nilivyowaambia, nikisema, Wapelelezi ninyi. 15 Mtabainika kwa njia hii; aishivyo Farao, hamtoki hapa, asipokuja huku huyo ndugu yenu mdogo. 16 Mpelekeni mmoja wenu, aende akamlete ndugu yenu, na ninyi mtafungwa, hata maneno yenu yahakikishwe, kama mna kweli ninyi; ikiwa sivyo, aishivyo Farao, ninyi ni wapelelezi. 17 Akawatia wote gerezani siku tatu. 18 Yusufu akawaambia siku ya tatu, Fanyeni hivi, mkaishi, maana mimi namcha Mungu. 19 Kama ni wa kweli ninyi ndugu yenu mmoja na afungwe gerezani, nanyi nendeni mkachukue nafaka kwa njaa ya nyumba zenu, 20 mkamlete ndugu yenu mdogo kwangu; hivyo maneno yenu yatahakikishwa, wala hamtakufa. Ndivyo walivyofanya. 21 Wakaambiana, Kweli sisi tulimkosa ndugu yetu, kwa kuwa tuliona shida ya roho yake, alipotusihi, wala hatukusikia kwa hiyo shida hii imetupata. 22 Reubeni akajibu, akawaambia, Sikuwaambia, nikisema, msimkose kijana? Wala hamkusikia; kwa hiyo damu yake inatakwa tena. 23 Wala hawakujua ya kwamba Yusufu anawasikia, kwa sababu alikuwapo mkalimani kati yao. 24 Akajitenga nao akalia. Kisha akawarudia, na kusema nao, akamtwaa Simeoni miongoni mwao, akamfunga mbele ya macho yao. 25 Yusufu akaamuru kuvijaza vyombo vyao nafaka, na kumrudishia kila mtu fedha yake katika gunia lake, na kuwapa chakula cha njiani. 26 Navyo ndivyo walivyofanyiwa. Wakaweka nafaka yao juu ya punda zao, wakatoka huko. 27 Mmoja wao alipofungua gunia lake ili ampe punda wake chakula katika nyumba ya wageni, aliiona fedha yake; kumbe! Iko kinywani mwa gunia lake. 28 Akawaambia nduguze, Fedha yangu imerudishwa, angalia, imo humo guniani mwangu. Mioyo yao ikazimia, wakageukiana wakitetemeka, wakasema, N'nini hii Mungu aliyotutendea? 29 Wakaja kwa Yakobo, baba yao, katika nchi ya Kanaani, wakampasha habari za yote yaliyowapata, wakisema, 30 Mtu yule aliye bwana wa nchi alisema nasi kwa maneno makali, akatufanya tu wapelelezi wa nchi. 31 Tukamwambia, Tu watu wa kweli sisi, wala si wapelelezi. 32 Sisi tu ndugu kumi na wawili, wana wa baba yetu. Mmoja hayuko, na mdogo wetu yuko pamoja na baba yetu leo katika nchi ya Kanaani. 33 Yule mtu, bwana wa nchi, akatuambia, Kwa njia hii nitawajua kama ninyi ni watu wa kweli; ndugu yenu mmoja mwacheni huku kwangu, kachukueni nafaka kwa njaa ya nyumba zenu, mwende zenu. 34 Mkaniletee ndugu yenu mdogo; ndipo nitakapojua kama ninyi si wapelelezi, bali ni watu wa kweli; basi nitawarudishia ndugu yenu, nanyi mtafanya biashara katika nchi hii. 35 Ikawa walipomimina magunia yao, kumbe! Bahasha ya fedha ya kila mtu imo katika gunia lake. Nao walipoziona bahasha za fedha zao, wao na baba yao waliogopa. 36 Yakobo baba yao akawaambia, Mmeniondolea watoto wangu; Yusufu hayuko, wala Simeoni hayuko, na Benyamini mnataka kumchukua naye; mambo hayo yote yamenipata mimi. 37 Reubeni akamwambia babaye, akasema, Uwaue wanangu wawili nisipomrudisha kwako; mtie katika mikono yangu, nami nitamrudisha kwako. 38 Akasema, Mwanangu hatashuka pamoja nanyi, maana nduguye amekufa, naye amesalia peke yake; mabaya yakimpata katika njia mtakayoiendea ndipo mtakaposhusha mvi zangu kwa sikitiko mpaka kaburini.

Mwanzo 43

1 Njaa ikawa nzito katika nchi. 2 Ikawa walipokwisha kula nafaka waliyoileta kutoka Misri, baba yao akawaambia, Rudini huko, mkatununulie chakula kidogo. 3 Yuda akamwambia akisema, Yule mtu alituagizia sana akisema, Hamtaniona uso wangu, ndugu yenu asipokuwa pamoja nanyi. 4 Ukimpeleka ndugu yetu pamoja nasi, tutashuka na kukununulia chakula. 5 Ila usipompeleka, hatushuki, maana mtu yule alituambia, Hamtaniona uso wangu, ndugu yenu asipokuwa pamoja nanyi. 6 Israeli akasema, Mbona mmenitendea vibaya hata mkamwarifu mtu yule ya kwamba mna ndugu mwingine? 7 Wakasema, Mtu yule alituhoji sana habari zetu na za jamaa yetu, akisema, Baba yenu angali hai? Mnaye ndugu mwingine? Nasi tukamjibu sawasawa na maswali hayo. Je! Tuliweza kujua ya kwamba atasema, Shukeni pamoja na ndugu yenu? 8 Yuda akamwambia Israeli babaye, Mpeleke kijana pamoja nami, tuondoke, tuende zetu, ili tupate kuishi, wala tusife, sisi na wewe na watoto wetu. 9 Mimi nitakuwa mdhamini wake, umtake mkononi mwangu. Nisipomleta tena kwako, na kumweka mbele yako, nitakuwa mwenye hatia mbele yako daima; 10 maana kama hatungalikawia, hakika tungaliisha kurudi mara ya pili. 11 Israeli, baba yao, akawaambia, Kama ndivyo, fanyeni hivi; twaeni tunu za nchi katika vyombo vyenu, mkamchukulie mtu huyo zawadi, zeri kidogo, na asali kidogo, ubani, na manemane, na jozi, na lozi. 12 Mkatwae fedha maradufu mikononi mwenu, na fedha zile zilizorudishwa kinywani mwa magunia yenu zirudisheni mikononi mwenu; labda zilisahauliwa. 13 Mtwaeni na ndugu yenu, mwondoke na kurudi kwa mtu yule. 14 Mungu Mwenyezi na awape rehema usoni pa mtu yule ili awafungulie ndugu yenu huyo mwingine, na Benyamini. Nami nikifiwa na watoto wangu, nimefiwa. 15 Basi hao watu wakatwaa zawadi ile, wakatwaa na fedha maradufu mikononi mwao, na Benyamini; wakaondoka, wakashuka mpaka Misri, wakasimama mbele ya Yusufu. 16 Naye Yusufu alipomwona Benyamini pamoja nao, akamwambia msimamizi wa nyumba yake, Uwalete watu hawa nyumbani, ukachinje na kuandalia, maana watu hawa watakula pamoja nami adhuhuri. 17 Yule mtu akafanya kama Yusufu alivyomwambia Naye akawaleta watu hao nyumbani mwa Yusufu. 18 Lakini watu hao wakaogopa kwa sababu wameletwa nyumbani mwa Yusufu, wakasema, Kwa sababu ya fedha zile zilizorudishwa katika magunia yetu mara ya kwanza tumeletwa humu; apate kutushitaki, na kutuangukia, atutwae sisi kuwa watumwa, na punda zetu. 19 Wakamkaribia yule msimamizi wa nyumba ya Yusufu, wakasema naye mlangoni pa nyumba. 20 Wakamwambia, Tazama, bwana, kweli tulishuka mara ya kwanza ili tununue chakula. 21 Ikawa, tulipofika nyumba ya wageni, tukafungua magunia yetu, kumbe! Fedha za kila mtu zilikuwako kinywani mwa gunia lake, fedha zetu kwa uzani wake kamili; nasi tumezileta tena mikononi mwetu. 22 Nasi tumeleta fedha nyingine mikononi mwetu ili tununue chakula; hatujui ni nani aliyezitia fedha zetu katika magunia yetu. 23 Akawaambia, Amani iwe kwenu, msiogope; Mungu wenu, naye ni Mungu wa baba yenu, amewapa akiba katika magunia yenu; fedha zenu ziliniwasilia. Kisha akawatolea Simeoni. 24 Mtu yule akawaleta wale watu nyumbani mwa Yusufu, akawapa maji, wakatawadha miguu, akawapa punda zao chakula. 25 Wakaiweka tayari ile zawadi hata atakapokuja Yusufu adhuhuri, maana wamesikia ya kwamba watakula chakula huko. 26 Alipokuja Yusufu nyumbani, wakamletea ile zawadi iliyokuwa mikononi mwao nyumbani mwake, wakamwinamia mpaka nchi. 27 Akawaulizia hali yao, akasema, Je! Baba yenu, yule mzee mliyemnena, hajambo? Angali hai? 28 Wakasema, Mtumwa wako baba yetu hajambo, angali hai; wakainama, wakasujudu. 29 Akainua macho yake, akamwona Benyamini, nduguye, mwana wa mamake, akasema, Huyu ndiye ndugu yenu mdogo, mliyeniambia habari zake? Akasema, Mungu akufadhili, mwanangu. 30 Yusufu akafanya haraka, kwa sababu moyo wake ulimwonea shauku nduguye, akatafuta pa kulia, akaingia chumbani mwake, akalia humo. 31 Akanawa uso, akatoka, akajizuia, akasema, Leteni chakula. 32 Wakamwandalia yeye peke yake, na wao peke yao, na wale Wamisri waliokula pamoja naye peke yao; maana Wamisri hawawezi kula pamoja na Waebrania, kwa kuwa ni chukizo kwa Wamisri. 33 Wakaketi mbele yake, mzaliwa wa kwanza kwa cheo cha kuzaliwa kwake, na mdogo kwa udogo wake; watu hao wakastaajabu wao kwa wao. 34 Wakapelekewa sehemu za chakula kutoka mezani pake, lakini akazidisha sehemu ya Benyamini iwe kubwa mara tano kuliko zao. Wakanywa, wakafanya furaha pamoja naye.

Mwanzo 44

1 Akamwamuru yule msimamizi wa nyumba yake akisema, Jaza magunia ya watu hawa chakula kwa kadiri wawezavyo kuchukua, utie na fedha ya kila mtu kinywani mwa gunia lake. 2 Na kikombe changu, kikombe kile cha fedha, ukitie kinywani mwa gunia la yule mdogo pamoja na fedha ya nafaka yake. Akafanya kama vile alivyomwambia Yusufu. 3 Asubuhi kulipopambazuka, hao watu wakapewa ruhusa, wao na punda zao. 4 Na walipotoka mjini, wala hawajaendelea sana, Yusufu akamwambia yule msimamizi wa nyumba yake, Ondoka, uwafuate watu hawa, nawe utakapowapata, waambie, Kwa nini mmelipa mabaya kwa mema? 5 Je! Kikombe hiki, sicho anyweacho bwana wangu? Naye hufanya uaguzi kwa hicho. Mmefanya vibaya kwa kufanya hivi. 6 Akawafuata, akawapata, na kuwaambia maneno hayo. 7 Wakamwambia, Kwa nini bwana wangu anasema maneno kama haya? 8 Hasha! Watumwa wako wasifanye hivi; tazama, hizo fedha mlizoziona kinywani mwa magunia yetu, tumekuletea tena kutoka nchi ya Kanaani. Tuwezeje sisi kuiba nyumbani mwa bwana wako fedha au dhahabu? 9 Atakayeonekana kuwa nacho miongoni mwa watumwa wako, na afe, na sisi nasi tutakuwa watumwa wa bwana wangu. 10 Akasema, Basi na iwe hivyo kama mlivyosema, Mtu atakayeonekana kuwa nacho atakuwa mtumwa wangu, na ninyi mtakuwa hamna hatia. 11 Wakafanya haraka, wakashusha kila mtu gunia lake, na kufungua kila mtu gunia lake. 12 Naye akatafuta, akaanza kwa mkubwa na kuisha kwa mdogo. Kikombe kikaonekana katika gunia la Benyamini. 13 Wakararua nguo zao, wakaweka kila mtu mzigo wake juu ya punda wake, wakarudi mjini. 14 Akaja Yuda na ndugu zake nyumbani kwa Yusufu, naye mwenyewe alikuwamo, nao wakamwangukia kifudifudi. 15 Yusufu akawaambia, Ni tendo gani hili mlilolitenda? Hamkujua ya kwamba mtu kama mimi naweza kufanya uaguzi? 16 Yuda akasema, Tumwambie nini bwana wangu? Tusemeje! Tujivutieje haki? Mungu ameona uovu wa watumwa wako. Tazama, sisi ni watumwa wa bwana wangu, sisi na yeye ambaye kikombe kilionekana mkononi mwake. 17 Akasema, Hasha! Nisifanye hivi; mtu ambaye kikombe kilionekana mkononi mwake, ndiye atakayekuwa mtumwa wangu. Nanyi enendeni zenu kwa amani kwa baba yenu. 18 Ndipo Yuda akamkaribia, akasema, Tafadhali, bwana wangu, mtumwa wako na aseme neno moja masikioni mwa bwana wangu, wala hasira yako isimwakie mtumwa wako, maana wewe u kama Farao. 19 Wewe, bwana wangu, ulituuliza watumwa wako, ukisema, Je! Mnaye baba, au ndugu? 20 Tukakuambia wewe, bwana wangu, Tunaye baba, naye ni mzee, na mwana wa uzee wake ni mdogo, na nduguye amekufa; amebaki yeye peke yake wa katika tumbo la mamaye, na baba yake anampenda. 21 Ukatuambia watumwa wako, Mleteni kwangu, ili macho yangu yamwangalie. 22 Tukakuambia, bwana wangu, Kijana hawezi kumwacha babaye, maana akimwacha babaye, babaye atakufa. 23 Ukatuambia watumwa wako, Asiposhuka ndugu yenu mdogo pamoja nanyi, hamtaniona uso wangu tena 24 Ikawa tulipokwenda kwa mtumwa wako, baba yangu, tukamwarifu maneno yako, bwana wangu. 25 Kisha baba yetu akanena, Rudini huko, mkatununulie chakula kidogo. 26 Tukasema, Hatuwezi kwenda; ndugu yetu mdogo akiwapo pamoja nasi, tutashuka, maana hatutaweza kuuona uso wa mtu huyo, ndugu yetu mdogo asipokuwa pamoja nasi. 27 Mtumwa wako, baba yangu, akatuambia, Mnajua ya kuwa mke wangu alinizalia wana wawili; 28 mmoja alitoka kwangu, nikasema, Bila shaka ameraruliwa, wala sikumwona tangu hapo. 29 Na mkiniondolea huyu naye, na madhara yakimpata, mtashusha mvi zangu na msiba kaburini. 30 Basi, nikienda kwa mtumwa wako, baba yangu, na huyu kijana hayupo pamoja nasi, iwapo roho yake imeshikamana na roho ya kijana; 31 itakuwa atakapoona ya kwamba huyu kijana hayuko, atakufa; na watumwa wako watashusha mvi za mtumwa wako, baba yetu, kwa huzuni kaburini. 32 Kwa maana mtumwa wako alijifanya mdhamini wa huyu kijana kwa baba yangu, nikisema, Nisipomrudisha kwako, nitakuwa na hatia kwa baba yangu sikuzote. 33 Basi, sasa nakusihi, uniache mimi mtumwa wako nikae badala ya huyu kijana kuwa mtumwa wa bwana wangu; na huyu kijana umwache aende pamoja na nduguze. 34 Kwa maana nitawezaje kumwendea baba yangu, na huyu kijana hayuko pamoja nami? Nisije nikayaona mabaya yatakayompata baba yangu.

Mwanzo 45

1 Hapo Yusufu hakuweza kujizuia mbele yao wote waliosimama karibu naye. Akapiga kelele, na kusema, Mwondoeni kila mtu mbele yangu. Wala hakusimama mtu pamoja naye, Yusufu alipojitambulisha kwa nduguze. 2 Akapaza sauti yake akalia, nao Wamisri wakasikia. Watu wa nyumba ya Farao nao wakasikia. 3 Yusufu akawaambia ndugu zake, Mimi ndimi Yusufu; baba yangu angali hai bado? Wala ndugu zake hawakuweza kumjibu, maana waliingiwa na hofu mbele yake. 4 Yusufu akawaambia ndugu zake, Karibuni kwangu; basi, wakakaribia. Akasema, Mimi ni Yusufu, ndugu yenu, ambaye mliniuza kwenda Misri. 5 Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa kuniuza huku; maana Mungu alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu. 6 Maana miaka hii miwili njaa imekuwa katika nchi, na iko tena miaka mitano isiyo na kulima wala kuvuna. 7 Mungu alinipeleka mbele yenu kuwahifadhia masazo katika nchi, na kuwaokoa ninyi kwa wokovu mkuu. 8 Basi si ninyi mlionipeleka huku, ila Mungu; naye ameniweka kama baba kwa Farao, na bwana katika nyumba yake yote, na mtawala katika nchi yote ya Misri. 9 Fanyeni haraka, mmwendee baba yangu, mkamwambie, Hivi ndivyo asemavyo mwanao Yusufu, Mungu ameniweka kuwa bwana katika Misri yote, basi unishukie, usikawie. 10 Nawe utakaa katika nchi ya Gosheni, utakuwa karibu nami, wewe, na wanao, na wana wa wanao, na wanyama wako, ng'ombe zako, na yote uliyo nayo. Nami nitakulisha huko; 11 maana bado imesalia miaka mitano ya njaa; usije ukaingia katika uhitaji, wewe, na nyumba yako, na yote uliyo nayo. 12 Na tazama, macho yenu yanaona, na macho ya ndugu yangu Benyamini, ya kwamba ni kinywa changu mimi kinachosema nanyi. 13 Nanyi mtamwarifu baba yangu habari za fahari yangu yote katika Misri, na za vyote mlivyoviona; mkafanye haraka kumleta huku baba yangu. 14 Akaanguka shingoni mwa ndugu yake Benyamini, akalia; Benyamini naye akalia shingoni mwake. 15 Akawabusu ndugu zake wote, akalia nao, baada ya hayo, nduguze wakazungumza naye 16 Habari ikasikika nyumbani mwa Farao kusema, Ndugu zake Yusufu wamekuja. Ikawa vema machoni pa Farao, na machoni pa watumwa wake. 17 Farao akamwambia Yusufu, Uwaambie ndugu zako, Fanyeni hivi; wachukuzeni mizigo wanyama wenu, mwondoke mwende nchi ya Kanaani; 18 kisha mkamtwae baba yenu, na watu wa nyumbani mwenu, mkanijie; nami nitawapa mema ya nchi ya Misri, nanyi mtakula unono wa nchi. 19 Nawe umeamriwa; fanyeni hivi, mjitwalie magari katika nchi ya Misri kwa watoto wenu wadogo na wake zenu, mkamchukue baba yenu mje. 20 Wala msivisumbukie vyombo vyenu, maana mema ya nchi yote ya Misri ni yenu. 21 Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. 22 Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. 23 Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. 24 Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani. 25 Wakatoka Misri, wakafika nchi ya Kanaani kwa Yakobo, baba yao. 26 Wakampasha habari, wakisema, Yusufu angali hai; naye ndiye mtawala katika nchi yote ya Misri. Moyo wake ukazimia, kwa sababu hakuwasadiki. 27 Wakamwambia maneno yote ya Yusufu, aliyowaambia; na alipoona magari aliyoyapeleka Yusufu, ili kumchukua, roho ya Yakobo baba yao ikafufuka. 28 Israeli akasema, Yatosha! Yusufu mwanangu angali hai; nitakwenda, nionane naye kabla sijafa.

Mwanzo 46

1 Akasafiri Israeli, pamoja na yote aliyokuwa nayo, akaja Beer-sheba, akamchinjia sadaka Mungu wa Isaka babaye. 2 Mungu akanena na Israeli katika ndoto ya usiku, akasema, Yakobo, Yakobo. Akasema, Mimi hapa. 3 Akasema, Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako, usiogope kushuka mpaka Misri; maana nitakufanya uwe taifa kubwa huko. 4 Mimi nitashuka pamoja nawe mpaka Misri; nami nitakupandisha tena bila shaka; na Yusufu ataweka mkono wake juu ya macho yako. 5 Yakobo akaondoka kutoka Beer-sheba; wana wa Israeli wakamchukua baba yao na watoto wao wadogo, na wake zao katika magari aliyoyapeleka Farao ili kumchukua. 6 Wakatwaa na wanyama wao, na mali zao walizokuwa wamezipata katika nchi ya Kanaani, wakaja Misri, Yakobo na uzao wake wote pamoja naye. 7 Wanawe, na wana wa wanawe, pamoja naye, binti zake na binti za wanawe, na uzao wake wote, aliwaleta pamoja naye mpaka Misri. 8 Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli walioingia Misri, Yakobo na wanawe: Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo. 9 Na wana wa Reubeni; Hanoki, na Palu, na Hesroni, na Karmi. 10 Na wana wa Simeoni; Yemueli na Yamini, na Ohadi, na Yakini, na Sohari, na Shauli, mwana wa mwanamke Mkanaani. 11 Na wana wa Lawi; Gershoni, na Kohathi, na Merari. 12 Na wana wa Yuda; Eri, na Onani, na Shela, na Peresi, na Zera; lakini Eri na Onani walikufa katika nchi ya Kanaani. Na wana wa Peresi, ni Hesroni, na Hamuli. 13 Na wana wa Isakari; Tola, na Puva, na Yashubu, na Shimroni. 14 Na wana wa Zabuloni; Seredi, na Eloni, na Yaleeli. 15 Hao ndio wana wa Lea, aliomzalia Yakobo katika Padan-aramu, na Dina, binti yake. Nafsi zote za wanawe na binti zake walikuwa thelathini na watatu. 16 Na wana wa Gadi; Sefoni, na Hagi, na Shuni, na Esboni, na Eri, na Arodi, na Areli. 17 Na wana wa Asheri; Imna, na Ishva, na Ishvi, na Beria, na Sera, umbu lao. Na wana wa Beria ni Heberi, na Malkieli. 18 Hao ndio wana wa Zilpa, ambaye Labani alimpa Lea, binti yake, naye akamzalia Yakobo hao, nafsi kumi na sita. 19 Wana wa Raheli, mkewe Yakobo Yusufu na Benyamini. 20 Walizaliwa kwake Yusufu katika nchi ya Misri, Manase na Efraimu, aliomzalia Asenathi binti Potifera, kuhani wa Oni. 21 Na wana wa Benyamini; Bela, na Bekeri, na Ashbeli, na Gera, na Naamani, na Ehi, na Roshi, na Mupimu, na Hupimu, na Ardi. 22 Hao ndio wana wa Raheli, aliomzalia Yakobo, nafsi zote walikuwa kumi na wanne. 23 Na wana wa Dani; Hushimu. 24 Na wana wa Naftali; Yaseeli, na Guni, na Yaseri, na Shilemu. 25 Hao ndio wana wa Bilha, ambaye Labani alimpa Raheli, binti yake, naye akamzalia Yakobo hao; nafsi zote walikuwa saba. 26 Nafsi zote waliokuja pamoja na Yakobo mpaka Misri waliotoka viunoni mwake, bila wake za wanawe Yakobo, nafsi zote walikuwa sitini na sita. 27 Na wana wa Yusufu aliozaliwa katika Misri walikuwa nafsi wawili. Nafsi zote za nyumba ya Yakobo walioingia Misri walikuwa sabini. 28 Yakobo akampeleka Yuda mbele yake kwa Yusufu, ili amwongoze njia mpaka Gosheni. Wakaja mpaka nchi ya Gosheni. 29 Yusufu akatandika gari lake, akapanda kwenda kumlaki Israeli, babaye, huko Gosheni; akajionyesha kwake, akamwangukia shingoni, akalia shingoni mwake kitambo kizima. 30 Israeli akamwambia Yusufu, Na nife sasa, kwa kuwa nimekuona uso wako, ya kuwa ungali hai. 31 Yusufu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumbani mwa baba yake, Nitapanda mimi nimpashe Farao habari; nitamwambia, Ndugu zangu, na watu wa nyumbani mwa baba yangu, waliokuwa katika nchi ya Kanaani, wamenijia. 32 Na watu hao ni wachungaji, maana wamekuwa watu wa kuchunga wanyama, nao wameleta kondoo zao, na ng'ombe zao, na yote waliyo nayo. 33 Itakuwa Farao atakapowaita, na kuwauliza, Kazi yenu ni nini? 34 Semeni, Watumwa wako tumekuwa wachunga wanyama tangu ujana wetu, na hata leo, sisi, na baba zetu; mpate kukaa katika nchi ya Gosheni; maana kila mchunga wanyama ni chukizo kwa Wamisri.

Mwanzo 47

1 Ndipo Yusufu akaja akamwarifu Farao, akasema, Baba yangu, na ndugu zangu, na kondoo zao, na ng'ombe zao, na yote waliyo nayo, wamekuja kutoka nchi ya Kanaani, nao wako katika nchi ya Gosheni. 2 Akatwaa watu watano miongoni mwa nduguze, akawasimamisha mbele ya Farao. 3 Farao akawauliza hao nduguze, Kazi yenu ni nini? Wakamwambia Farao, Watumwa wako tu wachunga wanyama, sisi, na baba zetu. 4 Wakamwambia Farao, Tumekuja kukaa ugenini katika nchi hii, kwa sababu wanyama wa watumwa wako hawana malisho, maana njaa ni nzito sana katika nchi ya Kanaani. Basi, twakusihi, uturuhusu sisi watumwa wako tukae katika nchi ya Gosheni. 5 Farao akamwambia Yusufu, akisema, Baba yako na ndugu zako wamekujia; 6 nchi ya Misri iko mbele yako, palipo pema pa nchi uwakalishe baba yako na ndugu zako; na wakae katika nchi ya Gosheni. Tena ukijua ya kuwa wako watu hodari miongoni mwao, uwaweke wawe wakuu wa wanyama wangu. 7 Yusufu akamleta Yakobo babaye ndani akamweka mbele ya Farao Yakobo akambariki Farao. 8 Farao akamwuliza Yakobo, Je! Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi? 9 Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao. 10 Yakobo akambariki Farao, akatoka mbele ya Farao. 11 Yusufu akawakalisha babaye na nduguze, na kuwapa milki katika nchi ya Misri, katika mahali pazuri pa nchi, katika nchi ya Ramesesi, kama Farao alivyoamuru. 12 Naye Yusufu akawalisha babaye na nduguze na nyumba yote ya babaye, kwa kadiri ya hesabu ya watoto wao. 13 Wala hapakuwa na chakula katika nchi yote, kwa kuwa njaa ilikuwa nzito sana, hata nchi ya Misri, na nchi ya Kanaani zikataabika, kwa sababu ya njaa. 14 Yusufu akakusanya fedha zote zilizoonekana katika nchi ya Misri na katika nchi ya Kanaani, kwa nafaka waliyoinunua. Yusufu akazileta zile fedha nyumbani mwa Farao. 15 Fedha zote zilipokwisha katika nchi ya Misri na katika nchi ya Kanaani, Wamisri wote walimjia Yusufu, wakisema, Tupe sisi chakula, kwa nini tufe mbele ya macho yako? Maana fedha zetu zimekwisha. 16 Yusufu akasema, Toeni wanyama wenu, nami nitawapa chakula badala ya wanyama wenu, kama fedha zenu zimekwisha. 17 Wakaleta wanyama wao kwa Yusufu; Yusufu akawapa chakula badala ya farasi, na badala ya kondoo, na badala ya ng'ombe, na badala ya punda, naye akawalisha chakula badala ya wanyama wao wote mwaka ule. 18 Na mwaka ule ulipokwisha wakamjia mwaka wa pili, wakamwambia, Hatumfichi bwana wetu ya kwamba fedha zetu zimekwisha, na makundi ya wanyama ni mali ya bwana wetu, hakikusalia kitu mbele ya bwana wetu, ila miili yetu na nchi zetu. 19 Kwa nini tufe mbele ya macho yako, sisi na nchi yetu? Utununue sisi na nchi yetu kwa chakula, na sisi na nchi yetu tutakuwa watumwa wa Farao; kisha utupe mbegu, tuishi wala tusife, wala nchi yetu isipotee. 20 Basi Yusufu akamnunulia Farao nchi yote ya Misri; maana Wamisri waliuza kila mtu shamba lake; kwa sababu njaa ilikuwa imewazidi sana, nchi ikawa mali yake Farao. 21 Akawahamisha hao watu, akawaweka katika miji, tangu upande huu wa Misri hata upande huu. 22 Ila nchi ya makuhani hakuinunua; maana makuhani walikuwa na posho yao kutoka kwa Farao, wakala posho yao waliyopewa na Farao. Kwa hiyo hawakuuza nchi yao. 23 Yusufu akawaambia watu, Angalieni, nimewanunua leo, ninyi, na nchi yenu, kuwa mali ya Farao; basi mbegu zenu ni hizi, zipandeni katika nchi. 24 Itakuwa wakati wa mavuno mtampa Farao sehemu ya tano, na sehemu nne zitakuwa zenu wenyewe, kuwa mbegu za nchi, na chakula chenu, na chakula chao waliomo nyumbani mwenu, na chakula cha watoto wenu. 25 Wakasema, Umetulinda hai, na tuone kibali machoni pa bwana wetu, nasi tutakuwa watumwa wa Farao. 26 Yusufu akaifanya sheria kwa habari ya nchi ya Misri hata leo, ya kwamba sehemu ya tano iwe mali ya Farao. Ila nchi ya makuhani tu haikuwa mali ya Farao. 27 Israeli akakaa katika nchi ya Misri, katika nchi ya Gosheni. Wakapata mali humo, wakaongezeka na kuzidi sana. 28 Yakobo akaishi katika nchi ya Misri miaka kumi na saba, basi siku za miaka ya maisha yake Yakobo ilikuwa miaka mia moja na arobaini na saba. 29 Siku za kufa kwake Israeli zikakaribia; akamwita mwanawe Yusufu, akamwambia, Kama nimeona kibali machoni pako, weka mkono wako chini ya paja langu, ukanifanyie rehema na kweli; nakusihi usinizike katika Misri. 30 Lakini nitakapolala pamoja na baba zangu, unichukue toka Misri, unizike katika kaburi lao. Akasema, Nitafanya kama ulivyosema. 31 Akanena, Niapie. Naye akamwapia. Israeli akajiinamisha kwenye mchago wa kitanda.

Mwanzo 48

1 Ikawa, baada ya mambo hayo, Yusufu akaambiwa, Tazama, baba yako hawezi; akawatwaa wanawe wawili, Manase na Efraimu, pamoja naye. 2 Naye akaarifiwa Yakobo ya kwamba, Angalia, mwanao Yusufu anakuja kwako. Israeli akajitia nguvu, akaketi juu ya kitanda. 3 Yakobo akamwambia Yusufu, Mungu Mwenyezi alinitokea huko Luzu, katika nchi ya Kanaani, akanibariki, 4 akaniambia, Mimi hapa, nitakuongezea uzao wako, na kukuzidisha, nami nitakufanya uwe kundi la mataifa; kisha nitawapa wazao wako nchi hii baada yako, iwe milki ya milele. 5 Basi sasa wanao wawili uliozaliwa katika nchi ya Misri kabla sijaja kwako Misri ni watoto wangu, yaani, Efraimu na Manase watakuwa wangu, kama Reubeni na Simeoni. 6 Na wazao wako utakaozaa baada ya hawa watakuwa wako; kwa jina la ndugu zao wataitwa katika urithi wao. 7 Na mimi nilipokuja kutoka Padan, Raheli akanifia katika nchi ya Kanaani, njiani, si mwendo mkubwa kabla ya kufika Efrathi. Nikamzika katika njia ya Efrathi, ndio Bethlehemu. 8 Israeli akawaona wana wa Yusufu, akasema, Ni nani hawa? 9 Yusufu akamwambia babaye, Hawa ni wanangu, Mungu alionipa hapa. Akasema, Tafadhali uwalete kwangu nami nitawabariki. 10 Na macho ya Israeli yalikuwa mazito kwa uzee, wala hakuweza kuona. Akawaleta kwake, naye akawabusu, na kuwakumbatia. 11 Israeli akamwambia Yusufu, Sikudhani ya kwamba nitakuona uso wako, na Mungu amenionyesha na uzao wako pia. 12 Yusufu akawatoa katika magoti yake, naye akainama kifudifudi 13 Yusufu akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. 14 Israeli akanyosha mkono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, huku akijua atiavyo mikono; maana Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. 15 Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha, maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, 16 naye Malaika aliyeniokoa na maovu yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi. 17 Yusufu alipoona kwamba babaye anaweka mkono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efraimu, ikawa vibaya machoni pake. Akauinua mkono wa babaye auondoe katika kichwa cha Efraimu, ili auweke juu ya kichwa cha Manase. 18 Yusufu akamwambia babaye, Sivyo, babangu, maana huyu ni mzaliwa wa kwanza; weka mkono wako wa kuume kichwani pake. 19 Babaye akakataa, akasema, Najua, mwanangu najua, yeye naye atakuwa taifa, yeye naye atakuwa mkuu; lakini ndugu yake mdogo atakuwa mkubwa kuliko yeye, na uzao wake watakuwa wingi wa mataifa. 20 Akawabariki siku ile akasema, Katika ninyi Waisraeli watabariki, wakisema, Mungu na akufanye kama Efraimu na Manase. Akamweka Efraimu mbele ya Manase. 21 Israeli akamwambia Yusufu, Angalia, mimi ninakufa, lakini Mungu atakuwa pamoja nanyi, naye atawarudisha mpaka nchi ya baba zenu. 22 Nami nimekupa wewe sehemu moja zaidi kuliko ndugu zako, niliyoitwaa katika mikono ya Waamori, kwa upanga wangu na upinde wangu.

Mwanzo 49

1 Yakobo akawaita wanawe, akasema, Kusanyikeni, ili niwaambie yatakayowapata siku za mwisho. 2 Kusanyikeni, msikie, enyi wana wa Yakobo, Msikilizeni Israeli, baba yenu. 3 Reubeni, u mzaliwa wangu wa kwanza, Nguvu zangu, na malimbuko ya uwezo wangu. Umewapita wengine kwa ukuu na kwa nguvu. 4 Umeruka mpaka kama maji, basi usiwe na ukuu, Kwa sababu ulikipanda kitanda cha baba yako, Ukakitia unajisi; alikipandia kitanda changu. 5 Simeoni na Lawi ni ndugu; Panga zao ni silaha za jeuri. 6 Nafsi yangu, usiingie katika siri yao, Fahari yangu usiungane na kusanyiko lao, Maana katika ghadhabu yao walimuua mtu, Na kwa ukaidi wao walikata mshipa wa ng'ombe; 7 Ghadhabu yao na ilaaniwe, maana ilikuwa kali, Na hasira yao, maana ilikuwa haina huruma. Nitawagawa katika Yakobo, Nitawatawanya katika Israeli. 8 Yuda, ndugu zako watakusifu, Mkono wako utakuwa shingoni mwa adui zako. Wana wa baba yako watakuinamia. 9 Yuda ni mwana-simba, Kutoka katika mawindo, mwanangu, umepanda; Aliinama akajilaza kama simba, Na kama simba mke; ni nani atakaye mwamsha? 10 Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, Wala mfanya sheria kati ya miguu yake, Hata atakapokuja Yeye, mwenye milki, Ambaye mataifa watamtii. 11 Atafunga punda wake katika mzabibu, Na mwana-punda wake katika mzabibu mzuri. Amefua nguo zake kwa mvinyo, Na mavazi yake kwa damu ya zabibu. 12 Macho yake yatakuwa mekundu kwa mvinyo, Na meno yake yatakuwa meupe kwa maziwa. 13 Zabuloni atakaa pwani ya bahari, Naye atakuwa kama pwani za kuegesha merikebu, Na mpaka wake utakuwa kando ya Sidoni. 14 Isakari ni punda hodari, Ajilazaye kati ya mazizi ya kondoo; 15 Akaona mahali pa raha, kuwa pema, Na nchi, ya kuwa ni nzuri, Akainama bega lake lichukue mizigo, Akawa mtumishi kwa kazi ngumu. 16 Dani atahukumu watu wake, Kama moja ya makabila ya Israeli; 17 Dani atakuwa nyoka barabarani, Bafe katika njia, Aumaye visigino vya farasi, Hata apandaye ataanguka chali. 18 Wokovu wako nimeungoja, Ee Bwana. 19 Gadi, jeshi litamsonga, Lakini atawasonga wao mpaka visigino. 20 Asheri, chakula chake kitakuwa kinono, Naye atatoa tunu za kifalme. 21 Naftali ni ayala aliyefunguliwa; Anatoa maneno mazuri. 22 Yusufu ni mti mchanga wenye kuzaa, Mti mchanga wenye kuzaa karibu na chemchemi, Matwi yake yametanda ukutani. 23 Wapiga mishale walimtenda machungu, Wakamtupia, wakamwudhi, 24 Lakini upinde wake ukakaa imara, Mikono yake ikapata nguvu, Kwa mikono ya Mwenye Enzi wa Yakobo; Kwa jina la mchungaji, yeye jiwe la Israeli, 25 Naam, kwa Mungu wa baba yako atakaye kusaidia; Kwa mibaraka ya mbinguni juu. Mibaraka ya vilindi vilivyo chini, Mibaraka ya maziwa, na ya mimba. 26 Mibaraka ya baba yako Imepita mibaraka ya milima ya kale, Vitu vinavyotamanika vya vilima vya milele; Na vikae juu ya kichwa cha Yusufu, Juu ya utosi wa kichwa chake aliye mkuu kati ya ndugu zake. 27 Benyamini ni mbwa-mwitu mwenye kurarua-rarua Asubuhi atakula mawindo, Na jioni atagawanya mateka. 28 Hizo zote ndizo kabila za Israeli kumi na mbili. Na hayo ndiyo aliyowaambia baba yao, na kuwabariki; mmoja mmoja kwa mbaraka wake aliwabariki. 29 Akawaamuru, akasema, Mimi ninakwenda kukusanywa pamoja na watu wangu; mnizike pamoja na baba zangu, katika pango iliyomo shambani mwa Efroni, Mhiti; 30 katika ile pango iliyomo shambani mwa Makpela, iliyo mbele ya Mamre katika nchi ya Kanaani, aliyoinunua Ibrahimu pamoja na shamba kwa Efroni Mhiti, pawe milki yake ya kuzikia. 31 Humo walimzika Ibrahimu, na Sara mkewe; humo wakamzika Isaka, na Rebeka mkewe; nami humo nikamzika Lea; 32 shamba na pango iliyomo lililonunuliwa kwa wazawa wa Hethi. 33 Basi Yakobo alipokwisha kuwaagiza wanawe, akakunja miguu yake kitandani, akafa, akakusanywa pamoja na watu wake.

Mwanzo 50

1 Yusufu akamwangukia babaye usoni, akamlilila, akambusu. 2 Yusufu akawaagiza watumishi wake waganga, kwamba wampake baba yake dawa asioze. Waganga wakampaka dawa Israeli. 3 Siku zake arobaini zikaisha, maana hivyo hutimizwa siku za kupaka dawa. Wamisri wakamlilia siku sabini. 4 Siku za kumlilia zilipopita, Yusufu alisema na watu wa nyumba ya Farao, akinena, Kama nimeona neema machoni penu, tafadhalini mkaseme masikioni mwa Farao, mkinena, Baba yangu aliniapisha, akisema, 5 Mimi ni katika kufa, unizike katika kaburi langu nililojichimbia katika nchi ya Kanaani. Basi tafadhali uniruhusu niende sasa nikamzike babangu, nami nitarudi. 6 Farao akasema, Uende, ukamzike baba yako, kama alivyokuapisha. 7 Basi Yusufu akaenda amzike babaye, na watumwa wote wa Farao wakaenda pamoja naye, wazee wa nyumbani mwake, na wazee wote wa nchi ya Misri. 8 Na nyumba yote ya Yusufu, na nduguze, na nyumba ya babaye; wakawaacha watoto wao tu, na kondoo zao, na ng'ombe zao, katika nchi ya Gosheni. 9 Kisha wakaenda pamoja naye wapanda farasi, na magari; wakawa jeshi kubwa sana. 10 Wakaja mpaka sakafu ya Atadi, iliyo ng'ambo ya Yordani. Wakaomboleza huko maombolezo makuu, mazito sana. Akafanya matanga ya babaye siku saba. 11 Nao waliokaa katika nchi, wale Wakanaani, walipoyaona matanga katika sakafu ya Atadi, wakasema, Matanga haya ya Wamisri ni makuu kwa hiyo mahali pale paliitwa Abel-Misri, iliyo ng'ambo ya Yordani. 12 Wanawe wakamfanyia kama alivyo waagiza; 13 kwa kuwa wanawe wakamchukuwa mpaka nchi ya Kanaani, nao wakamzika katika pango ya shamba la Makpela, iliyo mbele ya Mamre, aliyoinunua Ibrahimu pamoja na shamba kwa Efroni Mhiti, pawe milki yake pa kuzikia. 14 Yusufu akarudi Misri, yeye na ndugu zake, na wote waliyokwenda pamoja naye kumzika babaye, baada ya kumzika babaye. 15 Ndugu zake Yusufu walipoona ya kwamba baba yao amekufa, walisema, Labda Yusufu atatuchukia; naye atatulipa maovu yetu tuliyomtenda. 16 Wakapeleka watu kwa Yusufu, kunena, Baba yako alitoa amri kabla ya kufa kwake, akasema, 17 Mwambieni Yusufu hivi, Naomba uwaachilie ndugu zako kosa lao na dhambi yao, maana walikutenda mabaya; sasa twakuomba utuachilie kosa la watumwa wa Mungu wa baba yako. Yusufu akalia waliposema naye. 18 Nduguze wakaenda tena, wakamwangukia miguu, wakasema, Tazama, sisi tu watumwa wako. 19 Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? 20 Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo. 21 Basi sasa msiogope; mimi nitawalisha na watoto wenu. Akawafariji, na kusema nao vema. 22 Akakaa Yusufu katika Misri, yeye na nyumba ya babaye. Akaishi Yusufu miaka mia na kumi. 23 Yusufu akaona wana wa Efraimu hata kizazi cha tatu; na wana wa Makiri, mwana wa Manase, walizaliwa magotini mwa Yusufu. 24 Yusufu akawaambia nduguze, Mimi ninakufa, lakini Mungu atawajia ninyi bila shaka, atawapandisha toka nchi hii, mpaka nchi aliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo. 25 Yusufu akawaapisha wana wa Israeli, akasema, Bila shaka Mungu atawajia ninyi, nanyi mtaipandisha huko mifupa yangu. 26 Basi Yusufu akafa, mwenye miaka mia na kumi; wakampaka dawa, wakamtia katika sanduku, huko Misri.

Kutoka 1

1 Basi majina ya wana wa Israeli walioingia Misri ni haya; kila mtu pamoja na jamaa zake walikuja pamoja na Yakobo. 2 Reubeni, na Simeoni na Lawi, na Yuda; 3 na Isakari, na Zabuloni, na Benyamini; 4 na Dani, na Naftali, na Gadi, na Asheri. 5 Na nafsi zile zote zilizotoka viunoni mwa Yakobo zilikuwa ni nafsi sabini; na huyo Yusufu alikuwa huko ndani ya Misri tangu hapo. 6 Yusufu akafa, na ndugu zake wote, na watu wote wa kizazi kile. 7 Na wana wa Israeli walikuwa na uzazi sana, na kuongezeka mno, na kuzidi kuwa wengi, nao wakaendelea na kuongezeka nguvu; na ile nchi ilikuwa imejawa na wao. 8 Basi akainuka mfalme mpya kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. 9 Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. 10 Haya! Na tuwatendee kwa akili, wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii. 11 Basi wakaweka wasimamizi juu yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba, Pithomu na Ramesesi. 12 Lakini kwa kadiri ya walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka na kuzidi kuenea. Nao walichukiwa kwa sababu ya wana wa Israeli. 13 Wamisri wakawatumikisha wana wa Israeli kwa ukali; 14 wakafanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na ya matofali, na kila namna ya kazi ya mashamba; kwa kazi zao zote walizowatumikisha kwa ukali. 15 Kisha mfalme wa Misri akasema na wazalisha wa Waebrania, mmoja jina lake aliitwa Shifra, na wa pili jina lake aliitwa Pua; 16 akasema, Wakati mwazalishapo wanawake wa Kiebrania na kuwaona wa katika kuzaa, ikiwa ni mtoto mwanamume, basi mwueni, bali ikiwa ni mtoto mwanamke, na aishi. 17 Lakini wale wazalisha walikuwa wakimcha Mungu, wasifanye kama walivyoamriwa na huyo mfalme wa Misri, lakini wakawahifadhi hai wale wanaume. 18 Basi mfalme wa Misri akawaita wale wazalisha na kuwauliza, Kwa nini kufanya jambo hili, na kuwahifadhi watoto waume wawe hai? 19 Wazalisha wakamwambia Farao, Ni kwa sababu hao wanawake wa Kiebrania si kama wanawake wa Kimisri; kwa kuwa ni hodari hao, nao huzaa kabla mzalisha hajapata kuwafikilia. 20 Basi Mungu akawatendea mema wale wazalisha; na hao watu wakaongezeka sana, wakaendelea na kuzidi kuwa na nguvu nyingi. 21 Ilikuwa kwa sababu wale wazalisha walikuwa wakimcha Mungu, akawasimamishia nyumba. 22 Kisha huyo Farao akawaagiza watu wake, akisema, Kila mtoto mwanamume atakayezaliwa mtamtupa mtoni, na kila mtoto mwanamke mtamhifadhi hai.

Kutoka 2

1 Mtu mmoja wa nyumba ya Lawi akaondoka akaoa binti mmoja wa Lawi. 2 Yule mwanamke akachukua mimba akazaa mwana, na alipoona ya kuwa ni mtoto mzuri akamficha miezi mitatu. 3 Na alipokuwa hawezi kumficha tena, akampatia kisafina cha manyasi akakipaka sifa na lami, akamtia mtoto ndani yake, akakiweka katika majani kando ya mto. 4 Umbu lake mtoto akasimama mbali ili ajue yatakayompata. 5 Basi binti Farao akashuka, aoge mtoni, na vijakazi wake wakatembea kando ya mto; naye akakiona kile kisafina katika majani, akamtuma kijakazi wake kwenda kukileta. 6 Akakifungua, akamwona mtoto, na tazama, mtoto yule analia. Basi akamhurumia, akasema, Huyu ni mmojawapo wa watoto wa Waebrania. 7 Basi umbu lake mtoto akamwambia binti Farao, Je! Niende nikamwite mlezi katika wanawake wa Kiebrania, aje kwako, akunyonyeshee mtoto huyu? 8 Binti Farao akamwambia, Haya! Enenda. Yule kijana akaenda akamwita mama yake yule mtoto. 9 Binti Farao akamwambia, Mchukue mtoto huyu, ukaninyonyeshee, nami nitakupa mshahara wako. Yule mwanamke akamtwaa mtoto, akamnyonyesha. 10 Mtoto akakua, naye akamleta kwa binti Farao, akawa mwanawe. Akamwita jina lake Musa, akasema, Ni kwa sababu nalimtoa majini. 11 Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao. Akamwona Mmisri anampiga Mwebrania, mmojawapo wa ndugu zake. 12 Basi akatazama huko na huko, na alipoona ya kuwa hapana mtu, akampiga Mmisri yule, akamficha ndani ya mchanga. 13 Akatoka siku ya pili, na tazama, watu wawili wa Waebrania walikuwa wakipigana. Akamwambia yule aliyemdhulumu mwenzake, Mbona unampiga mwenzako? 14 Yule akasema, Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mkuu wetu, na mwamuzi juu yetu? Je! Wataka kuniua mimi kama ulivyomwua yule Mmisri? Musa akaogopa, akasema, Kumbe! Jambo lile limejulikana. 15 Basi Farao alipopata habari, akataka kumwua Musa; lakini Musa akakimbia mbele ya Farao, akakaa katika nchi ya Midiani; akaketi karibu na kisima. 16 Basi kuhani wa Midiani alikuwa na binti saba, nao wakaja wakateka maji, wakazijaza birika maji, wapate kunywesha kundi la baba yao. 17 Wachungaji wakaja wakawafukuza; lakini Musa akasimama, akawasaidia, akalinywesha kundi lao. 18 Walipofika kwa Reueli baba yao, akasema, Imekuwaje hata mkarejea mapema leo? 19 Wakasema, Mmisri mmoja alituokoa katika mikono ya wachungaji, tena zaidi ya hayo, akatutekea maji, akalinywesha kundi. 20 Akawaambia binti zake, Yuko wapi basi? Mbona mmemwacha mtu huyo? Mwiteni, ale chakula. 21 Musa akawa radhi kukaa kwake mtu yule, naye akampa Musa binti yake, Sipora. 22 Huyo akamzalia mwana, akamwita jina lake Gershomu, maana alisema, Nimekuwa mgeni katika nchi ya ugeni. 23 Hata baada ya siku zile nyingi mfalme wa Misri akafa; wana wa Israeli wakaugua kwa sababu ya ule utumwa, wakalia; kilio chao kikafika juu kwa Mungu kwa sababu ya ule utumwa. 24 Mungu akasikia kuugua kwao, Mungu akakumbuka agano lake alilolifanya na Ibrahimu na Isaka na Yakobo. 25 Mungu akawaona wana wa Israeli, na Mungu akawaangalia. Print this page Top | Next Chapter | Index | Home Full online version here [with search engine, multilingual display and audio Bible]

Kutoka 3

1 Basi huyo Musa alikuwa akilichunga kundi la Yethro mkwewe, kuhani wa Midiani; akaliongoza kundi nyuma ya jangwa, akafika mpaka mlima wa Mungu, hata Horebu. 2 Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea. 3 Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki hakiteketei. 4 Bwana alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa. 5 Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu. 6 Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu. 7 Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; 8 nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. 9 Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. 10 Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri. 11 Musa akamwambia Mungu, Mimi ni nani, hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli watoke Misri? 12 Akasema, Bila shaka mimi nitakuwa pamoja nawe; na dalili ya kuwa nimekutuma ndiyo hii; utakapokuwa umekwisha kuwatoa hao watu katika Misri, mtamwabudu Mungu katika mlima huu. 13 Musa akamwambia Mungu, Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n'nani? Niwaambie nini? 14 Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO;akasema,Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli;MIMI NIKO amenituma kwenu. 15 Tena Mungu akamwambia Musa, Waambie wana wa Israeli maneno haya, Bwana, Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote. 16 Enenda, ukawakusanye wazee wa Israeli pamoja, ukawaambie, Bwana, Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenitokea, akaniambia, Hakika nimewajilieni, tena nimeyaona mnayotendewa huko Misri; 17 Nami nimesema, Nitawapandisha kutoka katika mateso ya Misri na kuwaingiza katika nchi ya Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, nchi ijaayo maziwa na asali. 18 Nao watakusikia sauti yako; nawe utakwenda, wewe na wazee wa Israeli kwa mfalme wa Misri, na kumwambia, Bwana Mungu wa Waebrania, amekutana nasi; basi sasa twakuomba, tupe ruhusa twende mwendo siku tatu jangwani, ili tumtolee dhabihu Bwana Mungu wetu. 19 Nami najua ya kuwa huyo mfalme wa Misri hatawapa ruhusa mwende zenu, la, hata kwa mkono wa nguvu. 20 Nami nitaunyosha mkono wangu, na kuipiga Misri kwa ajabu zangu zote, nitakazofanya kati yake, kisha baadaye atawapa ruhusa kwenda. 21 Nami nitawapa watu hao kufadhiliwa mbele ya Wamisri; hata itakuwa, hapo mtakapokwenda zenu hamtakwenda kitupu; 22 Lakini kila mwanamke ataomba kwa jirani, na kwa huyo akaaye naye nyumbani, vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na mavazi; nanyi mtawavika wana wenu na binti zenu; nanyi mtawateka nyara Wamisri.

Kutoka 4

1 Musa akajibu akasema, Lakini, tazama, hawataniamini, wala hawataisikia sauti yangu; maana watasema, Bwana hakukutokea. 2 Bwana akamwambia, Ni nini hiyo uliyo nayo mkononi mwako? Akasema, Ni fimbo. 3 Akamwambia, Itupe chini; akaitupa chini, nayo ikawa nyoka; Musa akakimbia mbele yake. 4 Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako, kamshike mkia; (akaunyosha mkono wake akamshika, naye akageuka kuwa fimbo mkononi mwake;) 5 ili kwamba wapate kusadiki ya kwamba Bwana, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amekutokea. 6 Bwana akamwambia tena, Sasa tia mkono wako kifuani mwako. Akautia mkono wake kifuani mwake; naye alipoutoa, kumbe! Mkono wake ulikuwa una ukoma, umekuwa mweupe kama theluji. 7 Akasema, Tia mkono wako kifuani mwako tena. Akautia mkono wake kifuani mwake tena, na alipoutoa kifuani mwake, kumbe! Umerudia hali ya mwili wake. 8 Basi itakuwa, wasipokusadiki, wala kuisikiliza sauti ya ishara ya kwanza, wataisikiliza sauti ya ishara ya pili. 9 Kisha itakuwa wasipoamini hata ishara hizo mbili, wala kuisikiliza sauti yako, basi, yatwae maji ya mtoni uyamwage juu ya nchi kavu, na yale maji uyatwaayo mtoni yatakuwa damu juu ya nchi kavu. 10 Musa akamwambia Bwana Ee Bwana, mimi si msemaji, tokea zamani, wala tokea hapo uliposema na mtumishi wako; maana mimi si mwepesi wa kusema, na ulimi wangu ni mzito. 11 Bwana akamwambia, Ni nani aliyekifanya kinywa cha mwanadamu? Au ni nani afanyaye mtu kuwa bubu au kiziwi, au mwenye kuona, au kuwa kipofu? Si mimi, Bwana? 12 Basi sasa, enenda, nami nitakuwa pamoja na kinywa chako, na kukufundisha utakalolinena. 13 Akasema, Ee Bwana, nakuomba, tuma kwa mkono wake huyo utakayemtuma. 14 Hasira ya Bwana ikawaka juu ya Musa, akasema, Je! Hayuko Haruni, ndugu yako, Mlawi? Najua ya kuwa yeye aweza kusema vizuri. Pamoja na hayo, tazama, anakuja kukulaki; naye atakapokuona, atafurahi moyoni mwake. 15 Nawe utasema naye, na kuyatia maneno kinywani mwake; nami nitakuwa pamoja na kinywa chako, na pamoja na kinywa chake, na kuwafundisheni mtakayofanya. 16 Naye atakuwa msemaji wako kwa watu, hata yeye atakuwa mfano wa kinywa kwako, nawe utakuwa mfano wa Mungu kwake. 17 Nawe utatwaa fimbo hii mkononi mwako, na kwa hiyo utazifanya zile ishara. 18 Basi Musa akaenda na kurejea kwa Yethro mkwewe, na kumwambia, Nipe ruhusa niende, nakusihi, niwarudie hao ndugu zangu walioko Misri, nipate kuwaona kwamba wako hai hata sasa. Yethro akamwambia Musa, Haya, nenda kwa amani. 19 Bwana akamwambia Musa huko Midiani, Haya, nenda, karudi Misri; kwa kuwa wale watu wote waliokutaka uhai wako wamekwisha kufa. 20 Basi Musa akamchukua mkewe na wanawe, na kuwapandisha juu ya punda, naye akarudi mpaka nchi ya Misri; na Musa akaichukua ile fimbo ya Mungu mkononi mwake. 21 Bwana akamwambia Musa, Hapo utakaporudi Misri, angalia ukazifanye mbele ya Farao zile ajabu zote nilizozitia mkononi mwako; lakini nitaufanya mgumu moyo wake, naye hatawapa ruhusa hao watu waende zao. 22 Nawe umwambie Farao, Bwana asema hivi, Israeli ni mwanangu mimi, mzaliwa wa kwanza wangu; 23 nami nimekuambia, Mpe mwanangu ruhusa aende, ili apate kunitumikia, nawe umekataa kumpa ruhusa aende; angalia basi, mimi nitamwua mwanao, mzaliwa wa kwanza wako. 24 Ilikuwa walipokuwa njiani mahali pa kulala, Bwana akakutana naye akataka kumwua. 25 Ndipo Sipora akashika jiwe gumu na kuikata govi ya zunga la mwanawe, na kuibwaga miguuni pake akasema. Hakika wewe u bwana arusi wa damu kwangu mimi. 26 Basi akamwacha. Ndipo huyo mkewe akanena, U bwana arusi wa damu wewe, kwa ajili ya kutahiri. 27 Bwana akamwambia Haruni, Nenda jangwani uonane na Musa. Naye akaenda, akamkuta katika mlima wa Mungu, akambusu. 28 Musa akamwambia Haruni hayo maneno yote ya Bwana ambayo alimtuma aende nayo, na ishara hizo zote alizomwagiza. 29 Musa na Haruni wakaenda, wakawakusanya wazee wote wa watu wa Israeli. 30 Haruni akawaambia maneno yote Bwana aliyonena na Musa akazifanya zile ishara mbele ya watu. 31 Watu wakaamini, na waliposikia ya kuwa Bwana amewajilia wana wa Israeli, na ya kuwa ameyaona mateso yao, wakainama vichwa vyao wakasujudu.

Kutoka 5

1 Hata baadaye, Musa na Haruni wakaenda wakamwambia Farao, wakasema, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Wape watu wangu ruhusa waende, ili kunifanyia sikukuu jangwani. 2 Farao akasema, Bwana ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui Bwana, wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao. 3 Wakasema, Mungu wa Waebrania amekutana nasi; twakuomba, tupe ruhusa twende safari ya siku tatu jangwani, tumtolee dhabihu Bwana, Mungu wetu; asije akatupiga kwa tauni, au kwa upanga. 4 Mfalme wa Misri akawaambia Enyi Musa na Haruni, mbona mnawaachisha watu kazi zao? Enendeni zenu kwa mizigo yenu. 5 Kisha Farao akasema, Tazameni, watu wa nchi sasa ni wengi, nanyi mnawapumzisha, wasichukue mizigo yao. 6 Na siku ile ile Farao akawaamuru wasimamizi wa watu, na wanyapara wao, akisema, 7 Msiwape watu tena majani ya kufanyia matofali, kama mlivyofanya tangu hapo; na waende wakatafute majani wenyewe. 8 Lakini hesabu ya matofali waliyokuwa wakifanya tokea hapo, wawekeeni iyo hiyo, msiipunguze hata kidogo, kwa maana ni wavivu hao; kwa hiyo wanapiga kelele, wakisema, Tupe ruhusa twende kumtolea Mungu wetu dhabihu. 9 Wapeni watu hao kazi nzito zaidi, waitaabikie; wala wasiangalie maneno ya uongo. 10 Hao wasimamizi wa watu na wanyapara wao wakatoka, wakasema na watu, wakanena, Farao asema hivi, Mimi siwapi majani. 11 Enendeni wenyewe, jipatieni majani hapo mtakapoyaona; kwa maana kazi yenu haitapunguzwa hata kidogo. 12 Basi hao watu wakatawanyika katika nchi yote ya Misri ili wapate kukusanya matakataka ya mashamba badala ya majani. 13 Wasimamizi wao wakawahimiza, wakisema, Timizeni kazi zenu, shughuli zenu za kila siku, kama wakati ule majani yalipokuwapo. 14 Na wanyapara wa wana wa Israeli, ambao wasimamizi wa Farao wamewaweka juu yao, wakapigwa, wakiambiwa, Kwa nini hamkutimiza kazi yenu jana na leo; kwa kufanya matofali kama hapo kwanza? 15 Basi wanyapara wa wana wa Israeli wakaenda, wakamlilia Farao, wakisema, Mbona umetutendea hivi, sisi watumwa wako? 16 Watumwa wako hawapewi majani, nao wanatuambia, Fanyeni matofali; na tazama, watumwa wako wapigwa; lakini kosa hilo ni la watu wako mwenyewe. 17 Akasema, Wavivu ninyi; wavivu; kwa ajili hii mwasema, Tupe ruhusa twende kumtolea Bwana dhabihu. 18 Basi, enendeni sasa, mkafanye kazi; kwa maana hamtapewa majani, na pamoja na hayo mtaleta hesabu ile ile ya matofali. 19 Basi wanyapara wa wana wa Israeli wakaona ya kwamba wa katika hali mbaya, walipoambiwa, Hamtapunguza hesabu ya matofali yenu hata kidogo; ndizo shughuli zenu za kila siku. 20 Wakakutana na Musa na Haruni, waliokuwa wanasimama njiani, hapo walipotoka kwa Farao; 21 wakawaambia, Bwana awaangalie na kuamua; kwa kuwa mmefanya harufu yetu kuwa chukizo mbele ya Farao, na mbele ya watumishi wake, mkatia upanga mikononi mwao, watuue. 22 Musa akarudi kwa Bwana, akasema, Bwana, mbona umewatenda mabaya watu hawa? Kwani kunituma mimi? 23 Kwa maana tangu nilipokwenda kwa Farao, kusema naye kwa jina lako, amewatenda mabaya watu hawa; wala hukuwaokoa watu wako hata kidogo.

Kutoka 6

1 Bwana akamwambia Musa, Sasa utaona nitakavyomtenda Farao; maana kwa mkono hodari atawapa ruhusa kwenda zao, na kwa mkono hodari atawafukuza katika nchi yake. 2 Kisha Mungu akasema na Musa, akamwambia, Mimi ni YEHOVA; 3 nami nilimtokea Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kama Mungu Mwenyezi, bali kwa jina langu YEHOVA sikujulikana kwao. 4 Tena nimelithibitisha agano langu nao, la kuwapa nchi ya Kanaani; nchi ya kukaa kwao hali ya ugeni. 5 Na zaidi ya hayo, nimesikia kuugua kwao wana wa Israeli, ambao Wamisri wanawatumikisha, nami nimelikumbuka agano langu. 6 Basi waambie wana wa Israeli, Mimi ni YEHOVA, nami nitawatoa ninyi mtoke chini ya mizigo ya Wamisri, nami nitawaokoa na utumwa wao, nami nitawakomboa kwa mkono ulionyoshwa, na kwa hukumu kubwa; 7 nami nitawatwaeni kuwa watu wangu, nitakuwa Mungu kwenu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ni YEHOVA, Mungu wenu, niwatoaye mtoke chini ya mizigo ya Wamisri. 8 Nami nitawaleta hata nchi ile ambayo naliinua mkono wangu, niwape Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo; nitawapa iwe urithi wenu; Mimi ni YEHOVA. 9 Musa akawaambia wana wa Israeli maneno haya; lakini hawakumsikiliza Musa kwa ajili ya uchungu wa moyo, na kwa ajili ya utumwa mgumu. 10 Bwana akasema na Musa, akamwambia, 11 Ingia ndani, ukaseme na Farao, mfalme wa Misri, ili awape ruhusa wana wa Israeli watoke nchi yake. 12 Musa akanena mbele ya Bwana, akasema, Tazama, hao wana wa Israeli hawakunisikiza mimi; basi huyo Farao atanisikizaje, mimi niliye na midomo isiyo tohara? 13 Bwana akanena na Musa na Haruni, akawaagiza wawaendee wana wa Israeli, na Farao, mfalme wa Misri, ili awatoe hao wana wa Israeli katika nchi ya Misri. 14 Hawa ndio vichwa vya nyumba za baba zao: wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli; ni Hanoki, na Palu, na Hesroni, na Karmi; hao ni jamaa za Reubeni. 15 Na wana wa Simeoni; ni Yemueli, na Yamini, na Ohadi, na Yakini, na Sohari, na Shauli mwana wa mwanamke wa Kikanaani; hao ni jamaa za Simeoni. 16 Na haya ndiyo majina ya wana wa Lawi, sawasawa na vizazi vyao; Gershoni, na Kohathi, na Merari; na miaka ya maisha yake Lawi ilikuwa ni miaka mia na thelathini na saba. 17 Wana wa Gershoni; ni Libni, na Shimei, sawasawa na jamaa zao. 18 Na wana wa Kohathi; ni Amramu, na Ishari, na Hebroni, na Uzieli; na miaka ya maisha ya huyo Kohathi ilikuwa ni miaka mia na thelathini na mitatu. 19 Na wana wa Merari; ni Mali, na Mushi. Hizi ni jamaa za hao Walawi sawasawa na vizazi vyao. 20 Huyo Amramu akamwoa Yokebedi ndugu ya baba yake; naye akamzalia Haruni, na Musa; na miaka ya maisha yake Amramu ilikuwa ni miaka mia na thelathini na saba. 21 Na wana wa Ishari; ni Kora, na Nefegi, na Zikri. 22 Na wana wa Uzieli; ni Mishaeli, na Elisafani, na Sithri. 23 Haruni akamwoa Elisheba, binti ya Aminadabu, umbu lake Nashoni; naye akamzalia Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari. 24 Na wana wa Kora; ni Asiri, na Elkana, na Abiasafu; hizo ni jamaa za hao Wakora. 25 Na Eleazari mwana wa Haruni akamwoa mmoja miongoni mwa binti za Putieli; naye akamzalia Finehasi. Hawa ndio vichwa vya nyumba za mababa ya Walawi sawasawa na jamaa zao. 26 Hawa ni Haruni ye yule, na Musa ye yule, Bwana aliowaambia, akisema, Watoeni wana wa Israeli watoke nchi ya Misri sawasawa na majeshi yao. 27 Ni hao walionena na Farao mfalme wa Misri ili wawatoe wana wa Israeli watoke Misri; hao ni Musa ye yule, na Haruni ye yule. 28 Ilikuwa siku hiyo Bwana aliponena na Musa katika nchi ya Misri, 29 Bwana akamwambia Musa, akasema, Mimi ni Bwana; mwambie Farao mfalme wa Misri maneno yote nikuambiayo. 30 Musa akanena mbele ya Bwana, Mimi ni mtu mwenye midomo isiyo tohara, Farao atanisikizaje?

Kutoka 7

1 Bwana akamwambia Musa, Angalia, nimekufanya wewe kuwa kama Mungu kwa Farao; na huyo ndugu yako Haruni atakuwa nabii wako. 2 Utanena hayo yote nikuagizayo; na ndugu yako Haruni atanena na Farao, ili awape wana wa Israeli ruhusa watoke nchi yake. 3 Nami nitaufanya mgumu moyo wa Farao, nami nitazifanya kuwa nyingi ishara zangu na ajabu zangu katika nchi ya Misri. 4 Lakini Farao hatawasikiza ninyi, nami nitaweka mkono wangu juu ya Misri, na kuyatoa majeshi yangu, watu wangu, hao wana wa Israeli, watoke nchi ya Misri kwa hukumu zilizo kuu. 5 Na Wamisri watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, hapo nitakapounyosha mkono wangu juu ya Misri na kuwatoa wana wa Israeli watoke kati yao. 6 Musa na Haruni wakafanya vivyo; kama Bwana alivyowaambia, ndivyo walivyofanya. 7 Huyo Musa alikuwa ni mtu wa miaka themanini umri wake, na Haruni alikuwa ni mtu wa miaka themanini na mitatu, hapo waliponena na Farao. 8 Bwana akanena na Musa na Haruni, akawaambia, 9 Farao atakaponena nanyi, na kuwaambia, Jifanyieni miujiza; ndipo utakapomwambia Haruni, Shika fimbo yako, uibwage chini mbele ya Farao, ili iwe nyoka. 10 Basi Musa na Haruni wakaingia kwa Farao, wakafanya vivyo kama Bwana alivyowaambia; Haruni akaibwaga fimbo yake chini mbele ya Farao, mbele ya watumishi wake, ikawa nyoka. 11 Ndipo Farao naye akawaita wenye akili na wachawi; na hao waganga wa Misri wakafanya vivyo kwa uganga wao. 12 Wakabwaga chini kila mtu fimbo yake, nazo zikawa nyoka; lakini fimbo ya Haruni ikazimeza fimbo zao. 13 Moyo wa Farao ukawa ni mgumu asiwasikize; kama Bwana alivyonena. 14 Bwana akamwambia Musa, Moyo wa Farao ni mzito, anakataa kuwapa watu ruhusa waende zao. 15 Mwendee Farao asubuhi; tazama, atoka kwenda majini; nawe simama karibu na ufuo wa mto ili upate kuonana naye; na ile fimbo iliyogeuzwa kuwa nyoka utaichukua mkononi mwako. 16 Nawe umwambie, Bwana, Mungu wa Waebrania, amenituma nije kwako, kusema, Wape watu wangu ruhusa, ili wapate kunitumikia jangwani; nawe, tazama! Hujasikia hata sasa. 17 Bwana asema, Katika jambo hili utanijua ya kuwa mimi ndimi Bwana; tazama, nitayapiga haya maji yaliyo mtoni kwa fimbo hii niliyo nayo mkononi mwangu, nayo yatageuzwa kuwa damu. 18 Na hao samaki walio mtoni watakufa, na huo mto utatoa uvundo; nao Wamisri watachukizwa kuyanywa maji ya mtoni. 19 Bwana akamwambia Musa, Mwambie Haruni, Shika fimbo yako, kaunyoshe mkono wako juu ya maji ya Misri, juu ya mito yao, juu ya vijito vyao, na juu ya maziwa ya maji yao, na juu ya visima vyao vyote vya maji, ili yageuke kuwa damu, nako kutakuwa na damu katika nchi yote ya Misri, katika vyombo vya mti, na katika vyombo vya jiwe. 20 Musa na Haruni wakafanya hivyo, kama Bwana alivyowaambia; naye akaiinua ile fimbo, na kuyapiga maji yaliyokuwa mtoni, mbele ya Farao, mbele ya watumishi wake; na hayo maji yote yaliyokuwa katika mto yakageuzwa kuwa damu. 21 Hao samaki waliokuwa mtoni nao wakafa; na ule mto ukatoa uvundo, Wamisri wasipate kunywa maji ya mtoni; na ile damu ilikuwa katika nchi yote na Misri. 22 Lakini waganga wa Misri wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao; na moyo wake Farao ukawa mgumu, wala hakuwasikiza, kama Bwana alivyonena. 23 Farao akazunguka na kuingia nyumbani mwake, wala hata hilo hakuliweka moyoni. 24 Wamisri wote wakachimba-chimba kando ya mto ili wapate maji ya kunywa; maana, hawakuweza kuyanywa yale maji ya mtoni. 25 Zikatimia siku saba, baada ya Bwana kuupiga ule mto.

Kutoka 8

1 Bwana akamwambia Musa, Ingia kwa Farao, ukamwambie, Bwana asema hivi, Wape watu wangu ruhusa, ili wapate kunitumikia. 2 Tena kama ukikataa kuwapa ruhusa, tazama, nitaipiga mipaka yako yote kwa kuleta vyura; 3 na huo mto utafurika vyura, nao watakwea juu na kuingia ndani ya nyumba yako, na ndani ya chumba chako cha kulala, na juu ya kitanda chako, na ndani ya nyumba ya watumishi wako, na juu ya watu wako, na ndani ya meko yako, na ndani ya vyombo vyako vya kukandia unga. 4 Kisha hao vyura watakwea juu yako wewe, na juu ya watu wako, na juu ya watumishi wako wote. 5 Bwana akamwambia Musa, Mwambie Haruni, Nyosha mkono wako na fimbo yako juu ya mito, juu ya vijito, na juu ya maziwa ya maji, ukawalete vyura waje juu ya nchi yote ya Misri. 6 Basi Haruni akaunyosha mkono wake juu ya maji yote ya Misri; na hao vyura wakakwea juu, wakaifunika nchi ya Misri. 7 Waganga nao wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao; na kuwaleta vyura juu ya nchi ya Misri. 8 Ndipo Farao akawaita Musa na Haruni na kuwaambia, Mwombeni Bwana, ili awaondoe vyura hawa kwangu mimi na kwa watu wangu; nami nitawapa watu ruhusa waende zao, ili wamtolee Bwana dhabihu. 9 Musa akamwambia Farao, Haya, ujitukuze juu yangu katika jambo hili; sema ni lini unapotaka nikuombee wewe, na watumishi wako, na watu wako, ili hao vyura waangamizwe watoke kwako wewe na nyumba zako, wakae ndani ya mto tu. 10 Akamwambia, Kesho, Akasema, Na yawe kama neno lako; ili upate kujua ya kwamba hapana mwingine mfano wa Bwana, Mungu wetu. 11 Hao vyura wataondoka kutoka kwako wewe na nyumba zako, na watumishi wako, na watu wako; watasalia mtoni tu. 12 Basi Musa na Haruni wakatoka kwa Farao; Musa akamlilia Bwana katika jambo la hao vyura aliokuwa amewaleta juu ya Farao. 13 Bwana akafanya sawasawa na neno la Musa; na hao vyura wakafa kutoka katika zile nyumba, na katika viwanja, na katika mashamba. 14 Wakawakusanya chungu chungu; na nchi ikatoa uvundo. 15 Lakini Farao alipoona ya kuwa pana nafuu, akaufanya moyo wake kuwa mzito, asiwasikize; kama Bwana alivyonena. 16 Bwana akamwambia Musa, Mwambie Haruni, Nyosha fimbo yako, ukayapige mavumbi ya nchi, ili kwamba yawe chawa katika nchi yote ya Misri. 17 Nao wakafanya; Haruni akaunyosha mkono wake na fimbo yake, na kuyapiga mavumbi ya nchi, nayo yakawa chawa juu ya wanadamu na juu ya wanyama; mavumbi yote ya nchi yakawa ni chawa katika nchi yote ya Misri. 18 Hao waganga nao wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao, ili kwamba walete chawa, lakini wasiweze; nako kulikuwa na chawa juu ya wanadamu, na juu ya wanyama. 19 Ndipo wale waganga wakamwambia Farao, Jambo hili ni chanda cha Mungu; na moyo wake Farao ukawa mgumu asiwasikize; vile vile kama Bwana alivyonena. 20 Bwana akamwambia Musa, Inuka asubuhi na mapema usimame mbele ya Farao; angalia! Atoka aende majini; kamwambie, Bwana asema, Wape watu wangu ruhusa waende zao, ili wanitumikie mimi. 21 Au kwamba huwapi ruhusa watu wangu, tazama, nitaleta wingi wa mainzi juu yako wewe, na juu ya watumishi wako, na juu ya watu wako, nao wataingia ndani ya nyumba zako; na nyumba za Wamisri zitajawa na wingi wa mainzi, na nchi nayo ambayo wa juu yake. 22 Nami siku hiyo nitatenga nchi ya Gosheni, watu wangu wanayokaa, ili hao mainzi wasiwe huko; ili kwamba upate kujua wewe ya kuwa mimi ndimi Bwana kati ya dunia. 23 Nami nitatia mpaka kati ya watu wangu na watu wako; ishara hiyo italetwa kesho. 24 Bwana akafanya; wakaja wingi wa mainzi kwa uzito sana, wakaingia nyumbani mwa Farao, na katika nyumba za watumishi wake, tena katika nchi yote ya Misri; nayo nchi iliharibiwa kwa ajili ya wale mainzi. 25 Farao akawaita Musa na Haruni akawaambia, Endeni mkamtolee Mungu wenu dhabihu ndani ya nchi hii. 26 Musa akasema, Haitupasi kufanya hivyo; kwa kuwa tutamchinjia sadaka Bwana, Mungu wetu, na hayo machukizo ya Wamisri; je! Tutachinja sadaka ya hayo machukizo ya Wamisri mbele ya macho yao, wasitupige kwa mawe? 27 La, tutakwenda safari ya siku tatu jangwani, tumchinjie dhabihu Bwana, Mungu wetu, kama atakavyotuagiza. 28 Farao akasema, Mimi nitawapa ruhusa mwende, ili mmchinjie dhabihu Bwana, Mungu wenu, jangwani; lakini hamtakwenda mbali sana; haya niombeeni. 29 Musa akasema, Tazama, mimi natoka kwako, nami nitamwomba Bwana ili hao mainzi wamtoke Farao, na watumishi wake, na watu wake kesho; lakini Farao asitende kwa udanganyifu tena, kwa kutowaacha watu waende kumchinjia Bwana dhabihu. 30 Musa akatoka kwa Farao, akamwomba Bwana. 31 Bwana akafanya kama neno la Musa, akawaondoa wale mainzi wabaya kwake Farao, na kwa watumishi wake, na watu wake; hakusalia hata mmoja. 32 Farao akaufanya moyo wake kuwa mzito mara hiyo nayo, wala hakuwapa ruhusa hao watu waende zao.

Kutoka 9

1 Ndipo Bwana akamwambia Musa, Ingia wewe kwa Farao, umwambie, Bwana, Mungu wa Waebrania, yuasema, Wape ruhusa watu wangu ili waende wanitumikie. 2 Kwani ukikataa kuwapa ruhusa waende, na kuzidi kuwazuia, 3 tazama, mkono wa Bwana u juu ya wanyama wako wa mifugo walioko kondeni, juu ya farasi, na juu ya punda, na juu ya ngamia, na juu ya ng'ombe, na juu ya kondoo; kutakuwa na tauni nzito sana. 4 Kisha Bwana atawatenga wanyama wa Israeli na wanyama wa Misri; wala hakitakufa kitu cho chote cha wana wa Israeli. 5 Naye Bwana akaweka muda, akasema, Kesho Bwana atalifanya jambo hili katika nchi. 6 Bwana akalifanya jambo hilo siku ya pili, na wanyama wote wa kufugwa wa Misri wakafa; lakini katika wanyama wa wana wa Israeli hakufa hata mmoja. 7 Farao akatuma watu, na tazama, hapana mmoja aliyekufa katika wanyama wa wana wa Israeli. Lakini moyo wa Farao ulikuwa mzito, wala hakuwapa hao watu ruhusa waende zao. 8 Bwana akawaambia Musa na Haruni, Jitwalieni konzi za majivu ya tanuuni, kisha Musa na ayarushe juu kuelekea mbinguni mbele ya Farao. 9 Nayo yatakuwa ni mavumbi membamba juu ya nchi yote ya Misri, nayo yatakuwa majipu yenye kufura na kutumbuka juu ya wanadamu na juu ya wanyama, katika nchi yote ya Misri. 10 Basi wakatwaa majivu ya tanuuni, na kusimama mbele ya Farao; na Musa akayarusha juu mbinguni nayo yakawa ni majipu yenye kufura na kutumbuka juu ya wanadamu na juu ya wanyama. 11 Nao wale waganga hawakuweza kusimama mbele ya Musa kwa sababu ya hayo majipu, kwa maana hao waganga walikuwa na majipu, na Wamisri wote walikuwa nayo. 12 Bwana akaufanya mgumu moyo wa Farao, asiwasikize; vile vile kama Bwana alivyomwambia Musa. 13 Bwana akamwambia Musa, Ondoka asubuhi na mapema, ukasimame mbele ya Farao, umwambie, Bwana, Mungu wa Waebrania, asema, Wape watu wangu ruhusa waende ili wanitumikie. 14 Kwani wakati huu nitaleta mapigo yangu yote juu ya moyo wako, na juu ya watumishi wako, na juu ya watu wako; ili upate kujua ya kuwa hapana mmoja mfano wa mimi ulimwenguni mwote. 15 Kwa kuwa wakati huu ningekwisha kuunyosha mkono wangu, na kukupiga wewe na watu wako, kwa tauni, nawe ungekatiliwa mbali na kuondolewa katika nchi; 16 lakini, nilikusimamisha wewe kwa sababu hii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote. 17 Nawe, je! Hata sasa wajitukuza juu ya watu wangu, usiwape ruhusa waende zao? 18 Tazama, kesho wakati kama huu, nitanyesha mvua ya mawe nzito sana, ambayo mfano wake haujakuwa huko Misri tangu siku ile ilipoanza kuwa hata hivi sasa. 19 Basi sasa tuma wahimize waingie ndani wanyama wako na hayo yote uliyo nayo mashambani; kwani kila mtu na kila mnyama apatikanaye mashambani, wasioletwa nyumbani, hiyo mvua ya mawe itanyesha juu yao, nao watakufa. 20 Yeye aliyelicha neno la Bwana miongoni mwa watumishi wa Farao aliwakimbiza watumishi wake na wanyama wake waingie nyumbani; 21 na yeye asiyelitia moyoni neno la Bwana akawaacha watumishi wake na wanyama wake mashambani. 22 Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako kuelekea mbinguni, ili iwe mvua ya mawe katika nchi yote ya Misri, juu ya wanadamu na juu ya wanyama, na juu ya mboga zote za mashamba, katika nchi yote ya Misri. 23 Musa akaunyosha mkono wake kuelekea mbinguni; na Bwana akaleta ngurumo na mvua ya mawe, na moto ukashuka juu ya nchi; Bwana akanyesha mvua ya mawe juu ya nchi yote ya Misri. 24 Basi palikuwa na mvua ya mawe, na moto uliochanganyikana na ile mvua ya mawe, nzito sana, ambayo mfano wake haukuwapo katika nchi yote ya Misri tangu ilipoanza kuwa taifa. 25 Na ile mvua ya mawe ikapiga kila kilichokuwako mashambani, binadamu na mnyama, katika nchi yote ya Misri; hiyo mvua ya mawe ikapiga kila mmea wa mashambani, na kuuvunja kila mti wa mashamba. 26 Katika nchi ya Gosheni peke yake, walikokaa wana wa Israeli, haikuwako mvua ya mawe. 27 Farao akatuma watu, na kuwaita Musa na Haruni, na kuwaambia, Mimi nimekosa wakati huu; Bwana ni mwenye haki, na mimi na watu wangu tu waovu. 28 Mwombeni Bwana; kwa kuwa zimekuwa za kutosha ngurumo hizo kuu na hii mvua ya mawe; nami nitawapa ninyi ruhusa mwende zenu, msikae zaidi. 29 Musa akamwambia, Mara nitakapotoka mjini nitamwinulia Bwana mikono yangu; na hizo ngurumo zitakoma, wala haitanyesha mvua ya mawe tena; ili upate kujua ya kuwa dunia hii ni ya Bwana. 30 Lakini, wewe na watumishi wako, najua ya kuwa ninyi hamtamcha Bwana Mungu bado. 31 Kitani na shayiri zilipigwa; maana shayiri zilikuwa na masuke na kitani zilikuwa katika kutoa maua. 32 Lakini ngano na kusemethu hazikupigwa; maana, zilikuwa hazijakua bado. 33 Musa akatoka mjini, kutoka kwa Farao, akamwinulia Bwana mikono yake; na zile ngurumo na ile mvua ya mawe zikakoma, wala mvua haikunyesha juu ya nchi. 34 Farao alipoona ya kwamba mvua na mvua ya mawe na ngurumo zimekoma, akazidi kufanya dhambi, na kuufanya moyo wake mzito, yeye na watumishi wake. 35 Moyo wa Farao ukawa ni mgumu naye hakuwapa wana wa Israeli ruhusa waende zao; kama Bwana alivyonena kwa kinywa cha Musa.

Kutoka 10

1 Bwana akamwambia Musa, Ingia wewe kwa Farao; kwa kuwa mimi nimeufanya moyo wake mzito, nipate kuzionyesha ishara zangu hizi kati yao; 2 nawe upate kusema masikioni mwa mwanao, na masikioni mwa mjukuu wako, ni mambo gani niliyotenda juu ya Misri, na ishara zangu nilizozifanya kati yao; ili mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 3 Basi Musa na Haruni wakaingia kwa Farao, na kumwambia, Bwana, Mungu wa Waebrania, asema hivi, Je! Utakataa hata lini kujinyenyekeza mbele zangu? Wape watu wangu ruhusa waende zao, ili wanitumikie. 4 Au, kwamba wakataa kuwapa hao watu wangu ruhusa waende zao, tazama, kesho nitaleta nzige waingie ndani ya mipaka yako; 5 nao wataufunika uso wa nchi, mtu asipate kuona hiyo nchi; nao watakula mabaki ya hayo yaliyopona yaliyowasalia baada ya ile mvua ya mawe, watakula kila mti umeao kwa ajili yenu mashambani; 6 na nyumba zako, na nyumba za watumishi wako, na nyumba za Wamisri wote zitajawa na nzige; mfano wake baba zako wala baba za baba zako hawakuona, tangu siku walipoanza kuwapo juu ya nchi hata hivi leo. Basi akageuka na kutoka kwa Farao. 7 Ndipo watumishi wa Farao wakamwambia, Mtu huyu atakuwa tanzi kwetu sisi hata lini? Wape hawa watu ruhusa waende zao, wamtumikie Bwana, Mungu wao; hujatambua bado ya kuwa Misri imekwisha haribika? 8 Musa na Haruni wakaletwa tena kwa Farao; naye akawaambia, Nendeni, mkamtumikie Bwana, Mungu wenu; lakini ni kina nani watakaokwenda? 9 Musa akamjibu, Tutakwenda na vijana wetu na wazee wetu, na wana wetu, na binti zetu, tutakwenda na kondoo zetu na ng'ombe zetu; kwa kuwa inatupasa kumfanyia Bwana sikukuu. 10 Lakini akawaambia, Ehe, Bwana na awe pamoja nanyi, kama nitakavyowapa ruhusa kwenda zenu pamoja na watoto wenu; angalieni, kwa kuwa pana uovu huko mbele yenu. 11 Sivyo; endeni ninyi mlio watu wazima, mkamtumikie Bwana; kwa kuwa ndilo jambo mtakalo. Nao walifukuzwa usoni pa Farao. 12 Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako juu ya nchi ya Misri kwa hao nzige, ili wakwee juu ya nchi ya Misri, waile mimea yote ya nchi, yaani, vyote vilivyosazwa na ile mvua ya mawe. 13 Basi Musa akainyosha fimbo yake juu ya nchi ya Misri, na Bwana akaleta upepo kutoka mashariki juu ya nchi, mchana kutwa, na usiku kucha; kulipopambazuka ule upepo wa mashariki ukawaleta nzige. 14 Na hao nzige wakakwea juu ya nchi yote ya Misri, wakatua ndani ya mipaka yote ya Misri, walikuwa wabaya mno; hawajakuwapo nzige kama hao majira yo yote, wala baada yao hawatakuwa wengine jinsi hiyo. 15 Kwa kuwa waliufunika uso wote wa nchi, hata nchi iliingia giza; wakala mimea yote ya nchi, na matunda yote ya miti yaliyosazwa na ile mvua ya mawe; hapakusalia hata jani moja, mti wala mmea wa mashamba, katika nchi yote ya Misri. 16 Ndipo Farao akawaita Musa na Haruni haraka; akasema, Nimemfanyia dhambi Bwana, Mungu wenu na ninyi pia. 17 Basi sasa, nawasihi, nisameheni dhambi yangu mara hii moja tu, mkamwombe Bwana, Mungu wenu, aniondolee kifo hiki tu. 18 Akatoka kwa Farao, na kumwomba Bwana. 19 Bwana akaugeuza upepo wa magharibi wenye nguvu nyingi, ambao uliwaondoa wale nzige na kuwapeleka katika Bahari ya Shamu; hakusalia hata nzige mmoja ndani ya mipaka yote ya Misri. 20 Lakini Bwana akaufanya ule moyo wa Farao uwe mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa waende zao. 21 Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako kuelekea mbinguni, kuwe giza juu ya nchi ya Misri, watu wapapase-papase gizani. 22 Basi Musa akaunyosha mkono wake kuelekea mbinguni; kukawa na giza nene katika nchi yote ya Misri muda wa siku tatu; 23 hawakupata kuonana mtu na mwenziwe, wala hakuondoka mtu mahali alipokuwa muda wa siku tatu; lakini wana wa Israeli wote walikuwa na mwanga makaoni mwao. 24 Farao akamwita Musa, na kumwambia, Haya, nendeni, mkamtumikie Bwana; kondoo zenu na ng'ombe zenu tu na waachwe; watoto wenu nao na waende pamoja nanyi. 25 Musa akasema, Ni lazima utupe mikononi mwetu na wanyama wa dhabihu na wa sadaka za kuteketezwa, ili tupate kumchinjia Bwana Mungu wetu dhabihu. 26 Makundi yetu pia watakwenda pamoja nasi; hautasalia nyuma hata ukwato mmoja; kwa maana inampasa kutwaa katika hao tupate kumtumikia Bwana, Mungu wetu; nasi hatujui, hata tutakapofika huko, ni kitu gani ambacho kwa hicho inatupasa kumtumikia Bwana. 27 Lakini Bwana akaufanya kuwa mgumu moyo wa Farao, asikubali kuwapa ruhusa waende zao. 28 Farao akamwambia Musa, Nenda zako, ujiangalie, usinione uso tena; kwani siku hiyo utakayoniangalia uso wangu utakufa. 29 Musa akasema, Umenena vema; mimi sitakuangalia uso wako tena.

Kutoka 11

1 Bwana akamwambia Musa, Liko pigo moja bado, nitakaloleta juu ya Farao na juu ya Misri; baadaye atawapa ninyi ruhusa mtoke huku; naye hapo atakapowapa ruhusa, atawafukuza mtoke huku kabisa kabisa. 2 Basi nena wewe masikioni mwa watu hawa, na kila mtu mume na atake kwa jirani yake, na kila mwanamke atake kwa jirani yake, vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu. 3 Bwana akawapa watu hao kibali machoni pa Wamisri. Zaidi ya hayo, huyo Musa alikuwa ni mkuu sana katika nchi ya Misri, machoni pa watumishi wa Farao, na machoni pa watu wake. 4 Musa akasema, Bwana asema hivi, Kama usiku wa manane mimi nitatoka nipite kati ya Misri; 5 na wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri watakufa, tangu yule mzaliwa wa kwanza wa Farao aketiye katika kiti chake cha enzi, hata mzaliwa wa kwanza wa huyo kijakazi aliye pale nyuma ya jiwe la kusagia; na wazaliwa wa kwanza wote wa wanyama. 6 Ndipo kutakuwa na kilio kikuu katika nchi yote ya Misri, ambacho mfano wake haujakuwa bado majira yo yote, wala hautakuwako mfano wake tena kabisa. 7 Lakini katika wana wa Israeli hapana hata mbwa atakayetoa ulimi juu yao, juu ya mtu wala juu ya mnyama; ili kwamba mpate kujua jinsi Bwana anavyowatenga Wamisri na Waisraeli. 8 Tena hao watumishi wako wote watanitelemkia kwangu mimi, nao watanisujudia, wakisema, Toka wewe, na hawa watu wote wakufuatao; na baada ya hayo nitatoka. Basi akatoka kwa Farao na hasira kuu. 9 Bwana akamwambia Musa, Farao hatawasikiza ninyi; kusudi ajabu zangu ziongezeke katika nchi ya Misri. 10 Musa na Haruni walifanya ajabu hizo zote mbele ya Farao; Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, asiwape wana wa Israeli ruhusa watoke nchi yake.

Kutoka 12

1 Bwana akanena na Musa na Haruni katika nchi ya Misri, akawaambia, 2 Mwezi huu utakuwa mwanzo wa miezi kwenu; utakuwa ni mwezi wa kwanza wa mwaka kwenu. 3 Semeni na mkutano wote wa Israeli, mkawaambie, Siku ya kumi ya mwezi huu kila mtu atatwaa mwana-kondoo, kwa hesabu ya nyumba ya baba zao, mwana-kondoo kwa watu wa nyumba moja; 4 na ikiwa watu wa nyumba ni wachache kwa mwana-kondoo, basi yeye na jirani yake aliye karibu na nyumba yake na watwae mwana-kondoo mmoja, kwa kadiri ya hesabu ya watu; kwa kadiri ya ulaji wa kila mtu, ndivyo mtakavyofanya hesabu yenu kwa yule mwana-kondoo. 5 Mwana-kondoo wenu atakuwa hana ila, mume wa mwaka mmoja; mtamtwaa katika kondoo au katika mbuzi. 6 Nanyi mtamweka hata siku ya kumi na nne ya mwezi ule ule; na kusanyiko lote la mkutano wa Israeli watamchinja jioni. 7 Nao watatwaa baadhi ya damu yake na kuitia katika miimo miwili na katika kizingiti cha juu, katika zile nyumba watakazomla. 8 Watakula nyama yake usiku ule ule, imeokwa motoni, pamoja na mkate usiotiwa chachu; tena pamoja na mboga zenye uchungu. 9 Msiile mbichi, wala ya kutokoswa majini, bali imeokwa motoni; kichwa chake pamoja na miguu yake, na nyama zake za ndani. 10 Wala msisaze kitu chake cho chote hata asubuhi, bali kitu kitakachosalia hata asubuhi mtakichoma kwa moto. 11 Tena mtamla hivi; mtakuwa mmefungwa viuno vyenu, mmevaa viatu vyenu miguuni, na fimbo zenu mikononi mwenu; nanyi mtamla kwa haraka; ni pasaka ya Bwana. 12 Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, wa mwanadamu na wa mnyama; nami nitafanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri; Mimi ndimi Bwana. 13 Na ile damu itakuwa ishara kwenu katika zile nyumba mtakazokuwamo; nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lo lote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri. 14 Na siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaifanya iwe sikukuu kwa Bwana; mtaifanya iwe sikukuu katika vizazi vyenu vyote, kwa amri ya milele 15 Mtakula mikate isiyochachwa muda wa siku saba; siku hiyo ya kwanza mtaondoa chachu yote isiwe katika nyumba zenu kabisa; kwa kuwa mtu ye yote atakayekula mkate uliochachwa tangu siku hiyo ya kwanza hata siku ya saba, nafsi hiyo atakatiliwa mbali na Israeli. 16 Siku ya kwanza kutakuwa kwenu na kusanyiko takatifu, na siku ya saba kutakuwa kusanyiko takatifu; haitafanywa kazi yo yote katika siku hizo, isipokuwa kwa hiyo ambayo kila mtu hana budi kula, hiyo tu ifanyike kwenu. 17 Nanyi mtaitunza ile sikukuu ya mikate isiyochachwa; kwa kuwa katika siku iyo hiyo mimi nimeyatoa majeshi yenu katika nchi ya Misri; kwa hiyo mtaitunza siku hiyo katika vizazi vyenu vyote, kwa amri ya milele. 18 Mwezi wa kwanza, siku ya mwezi kumi na nne, wakati wa jioni, mtakula mikate isiyochachwa, hata siku ya mwezi ishirini na moja jioni. 19 Muda wa siku saba isionekane chachu katika nyumba zenu kabisa; kwa kuwa mtu ye yote atakayekula hiyo iliyotiwa chachu, nafsi hiyo atakatiliwa mbali na mkutano wa Israeli, akiwa mwenye kukaa hali ya ugeni, au akiwa mtu aliyezaliwa katika nchi. 20 Msile kitu chochote kilichochachwa; mtakula mikate isiyochachwa katika makao yenu yote. 21 Hapo ndipo Musa akawaita wazee wa Israeli, na kuwaambia, Nendeni, mkajitwalie wana-kondoo kama jamaa zenu zilivyo mkamchinje pasaka. 22 Nanyi twaeni tawi la hisopu, mkalichovye katika ile damu iliyo bakulini na kukipiga kizingiti cha juu, na miimo miwili ya mlango, kwa hiyo damu iliyo katika bakuli; tena mtu ye yote miongoni mwenu asitoke mlangoni mwa nyumba yake hata asubuhi. 23 Kwa kuwa Bwana atapita ili awapige hao Wamisri; na hapo atakapoiona hiyo damu katika kizingiti cha juu, na katika ile miimo miwili, Bwana atapita juu ya mlango, wala hatamwacha mwenye kuharibu aingie nyumbani mwenu kuwapiga ninyi. 24 Nanyi mtalitunza jambo hili kuwa ni amri kwako na kwa wanao milele. 25 Itakuwa hapo mtakapoifikilia hiyo nchi, Bwana atakayowapa, kama alivyoahidi, ndipo mtakapoushika utumishi huu. 26 Kisha itakuwa, hapo watoto wenu watakapowauliza, N'nini maana yake utumishi huu kwenu? 27 Ndipo mtawaambia, Ni dhabihu ya pasaka ya Bwana, kwa kuwa alipita juu ya nyumba za wana wa Israeli huko Misri, hapo alipowapiga Wamisri, akaziokoa nyumba zetu. Hao watu wakainama vichwa na kusujudia. 28 Basi wana wa Israeli wakaenda na kufanya mambo hayo; vile vile kama Bwana alivyowaamuru Musa na Haruni, ndivyo walivyofanya. 29 Hata ikawa, usiku wa manane Bwana akawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, tangu mzaliwa wa kwanza wa Farao aliyeketi katika kiti chake cha enzi, hata mzaliwa wa kwanza wa mtu aliyefungwa katika nyumba ya wafungwa; na wazaliwa wa kwanza wote wa wanyama. 30 Farao akaondoka usiku, yeye na watumishi wake wote, na Wamisri wote; pakawa na kilio kikuu katika Misri; maana hapakuwa na nyumba hata moja asimokufa mtu. 31 Akawaita Musa na Haruni usiku, akasema, Ondokeni tokeni katika watu wangu, ninyi na wana wa Israeli; enendeni, kamtumikieni Bwana kama mlivyosema. 32 Twaeni kondoo zenu na ng'ombe zenu kama mlivyosema, enendeni zenu, mkanibariki mimi pia. 33 Wamisri nao wakawahimiza watu, kuwatoa katika nchi kwa haraka, maana walisema, Tumekwisha kufa sote. 34 Watu wakauchukua unga wa mikate yao kabla haijatiwa chachu, na vyombo vyao vya kukandia wakavitia ndani ya nguo zao mabegani. 35 Wana wa Israeli wakafanya kama neno lile la Musa; wakataka kwa Wamisri vyombo vya fedha na vyombo vya dhahabu, na mavazi. 36 Bwana akawajalia kupendelewa na Wamisri hata wakawapa kila walichokitaka. Nao wakawateka Wamisri nyara. 37 Wana wa Israeli wakasafiri kutoka Ramesesi mpaka Sukothi, walipata hesabu yao kama watu sita mia elfu watu waume waliokwenda kwa miguu, bila kuhesabu watoto. 38 Na kundi kubwa la watu waliochangamana mno wakakwea pamoja nao; na kondoo na ng'ombe, wanyama wengi sana. 39 Nao wakaoka mikate isiyochachwa ya ule unga waliouchukua walipotoka Misri, maana, haukutiwa chachu, kwa sababu walitolewa watoke Misri, wasiweze kukawia, nao walikuwa hawajajifanyia tayari chakula. 40 Basi wana wa Israeli kukaa kwao, maana, muda waliokaa ndani ya Misri, ulikuwa ni miaka mia nne na thelathini. 41 Ilikuwa mwisho wa miaka hiyo mia nne na thelathini, ilikuwa siku ile ile, ya kwamba majeshi yote ya Bwana yalitoka nchi ya Misri. 42 Ni usiku wa kuangaliwa sana mbele za Bwana kwa sababu ya kuwatoa katika nchi ya Misri; huu ndio usiku wa Bwana, ambao wapasa kuangaliwa sana na wana wa Israeli wote katika vizazi vyao. 43 Bwana akawaambia Musa na Haruni, Amri ya pasaka ni hii; mtu mgeni asimle; 44 lakini mtumishi wa mtu awaye yote aliyenunuliwa kwa fedha, ukiisha kumtahiri, ndipo hapo atamla pasaka. 45 Akaaye kwenu hali ya ugeni, na mtumishi aliyeajiriwa, wasimle pasaka. 46 Na aliwe ndani ya nyumba moja; usiichukue nje ya nyumba nyama yake yo yote; wala msivunje mfupa wake uwao wote. 47 Na wafanye jambo hili mkutano wa Israeli wote. 48 Na mgeni atakapoketi pamoja nawe, na kupenda kumfanyia Bwana pasaka, waume wake wote na watahiriwe, ndipo hapo akaribie na kufanya pasaka; naye atakuwa mfano mmoja na mtu aliyezaliwa katika nchi; lakini mtu ye yote asiyetahiriwa asimle. 49 Sheria ni hiyo moja kwa mtu aliyezaliwa kwenu, na kwa mgeni akaaye kati yenu ugenini. 50 Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli wote; kama Bwana alivyowaagiza Musa na Haruni, ndivyo walivyofanya. 51 Ilikuwa siku ile ile moja, Bwana akawatoa wana wa Israeli katika nchi ya Misri kwa majeshi yao.

Kutoka 13

1 Bwana akasema na Musa, akamwambia, 2 Nitakasie mimi wazaliwa wa kwanza wote, kila afunguaye tumbo katika wana wa Israeli, wa binadamu na wa mnyama; ni wangu huyo. 3 Musa akawaambia hao watu, Kumbukeni siku hii, mliyotoka nchi ya Misri, kutoka nyumba ya utumwa; kwa kuwa Bwana aliwatoa mahali hapa kwa nguvu za mkono wake; na usiliwe mkate uliochachwa. 4 Ninyi mwatoka leo katika mwezi wa Abibu. 5 Itakuwa hapo Bwana atakapowaleta mpaka nchi ya Wakanaani, na Wahiti, na Waamori, na Wahivi, na Wayebusi, nchi hiyo aliyowaapia baba zako kwamba atakupa wewe, ni nchi imiminikayo maziwa na asali, ndipo mtakapoushika utumishi huu katika mwezi huu. 6 Mtakula mikate isiyochachwa muda wa siku saba, nayo siku ya saba itakuwa ni sikukuu ya Bwana. 7 Mikate isiyochachwa italiwa katika hizo siku saba; mkate uliotiwa chachu usionekane kwako, wala chachu isionekane kwako, ndani ya mipaka yako yote. 8 Nawe utamwambia mwanao siku hiyo, ukisema, Ni kwa sababu ya hayo Bwana aliyonifanyia hapo nilipotoka Misri. 9 Nayo itakuwa ishara kwako katika mkono wako, na kwa ukumbusho kati ya macho yako, ili kwamba sheria ya Bwana ipate kuwa kinywani mwako; kwani Bwana alikutoa utoke Misri kwa mkono wenye uwezo. 10 Kwa hiyo utaitunza amri hii kwa wakati wake mwaka baada ya mwaka. 11 Itakuwa hapo Bwana atakapokuleta katika nchi ya Wakanaani, kama alivyokuapia wewe na baba zako, na kukupa, 12 ndipo utamwekea Bwana kila afunguaye tumbo, na kila mzaliwa wa kwanza uliye naye, azaliwaye na mnyama; hao waume watakuwa ni wa Bwana. 13 Kila mzaliwa wa kwanza wa punda utamkomboa kwa mwana-kondoo; na kwamba hutaki kumkomboa, utamvunja shingo; na kila mzaliwa wa kwanza wa binadamu katika wanao utamkomboa. 14 Kisha itakuwa hapo mwanao atakapokuuliza keshoni, akisema, Ni nini hivi? Utamwambia, Bwana alimtoa Misri, kutoka ile nyumba ya utumwa, kwa uwezo wa mkono wake; 15 basi ilikuwa hapo Farao alipojifanya kuwa mgumu ili asitupe ruhusa kuondoka, Bwana akawapiga wazaliwa wa kwanza wote waliokuwa katika nchi ya Misri, wa binadamu na wa mnyama; kwa ajili ya hayo namtolea Bwana wote wafunguao tumbo, wakiwa waume; lakini wazaliwa wa kwanza wote wa wana wangu nawakomboa. 16 Jambo hilo litakuwa ni ishara mkononi mwako, na utepe katikati ya macho yako; kwa kuwa Bwana alitutoa Misri kwa uwezo wa mkono wake. 17 Ilikuwa hapo Farao alipokwisha kuwaacha watu hao waende zao, Mungu hakuwaongoza kwa njia ya nchi ya Wafilisti, ijapokuwa ilikuwa ni ya karibu; maana Mungu alisema, Wasije wakaghairi watu hawa hapo watakapokutana na vita, na kurudi Misri; 18 lakini Mungu akawazungusha hao watu kwa njia ya bara kando ya Bahari ya Shamu; wana wa Israeli wakakwea kutoka nchi ya Misri hali wamevaa silaha. 19 Musa akaichukua ile mifupa ya Yusufu pamoja naye; maana, alikuwa amewaapisha sana wana wa Israeli, akisema, Mungu hana budi atawajilia ninyi; nanyi mtaichukua mfupa yangu kutoka hapa pamoja nanyi. 20 Nao wakasafiri kutoka Sukothi, wakapiga kambi Ethamu, kwenye mpaka wa ile jangwa. 21 Bwana naye akawatangulia mchana ndani ya wingu mfano wa nguzo, ili awaongoze njia; na usiku, ndani ya moto mfano wa nguzo, ili kuwapa nuru; wapate kusafiri mchana na usiku; 22 ile nguzo ya wingu haikuondoka mchana, wala ile nguzo ya moto haikuondoka usiku, mbele ya hao watu.

Kutoka 14

1 Bwana akasema na Musa, akamwambia, 2 Waambie wana wa Israeli, kwamba warudi na kupiga kambi yao mbele ya Pi-hahirothi, kati ya Migdoli na bahari, kukabili Baal-sefoni; mtapanga mbele yake karibu na bahari. 3 Naye Farao atasema katika habari za wana wa Israeli, Wametatanishwa katika nchi, ile jangwa imewazuia wasitoke. 4 Nami nitaufanya uwe mgumu moyo wa Farao, naye atafuata nyuma yao; nami nitajipatia utukufu kwa Farao, na kwa jeshi lake lote; na Wamisri watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. Basi wakafanya hivyo. 5 Mfalme wa Misri aliambiwa ya kuwa wale watu wamekwisha kimbia; na moyo wa Farao, na mioyo ya watumishi wake, iligeuzwa iwe kinyume cha hao watu, nao wakasema, Ni nini jambo hili tulilotenda, kwa kuwaacha Waisraeli waende zao wasitutumikie tena? 6 Akaandalia gari lake, akawachukua watu wake pamoja naye; 7 tena akatwaa magari mia sita yaliyochaguliwa, na magari yote ya Wamisri, na maakida juu ya magari hayo yote. 8 Na Bwana akaufanya moyo wake Farao mfalme wa Misri kuwa mgumu, naye akawafuata wana wa Israeli; kwa sababu wana wa Israeli walitoka kwa ujeuri. 9 Wamisri wakafuata nyuma yao, farasi zote na magari yote ya Farao, na askari zake wenye kupanda farasi, na jeshi lake, nao wakawapata hali wamepanga pale karibu na bahari, karibu na Pi-hahirothi, kukabili Baal-sefoni. 10 Hata Farao alipokaribia, wana wa Israeli wakainua macho yao, na tazama, Wamisri wanakuja nyuma yao; wakaogopa sana; wana wa Israeli wakamlilia Bwana. 11 Wakamwambia Musa, Je! Kwa sababu hapakuwa na makaburi katika Misri umetutoa huko ili tufe jangwani? Mbona umetutendea haya, kututoa katika nchi ya Misri? 12 Neno hili silo tulilokuambia huko Misri, tukisema, Tuache tuwatumikie Wamisri? Maana ni afadhali kuwatumikia Wamisri kuliko kufa jangwani. 13 Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa Bwana atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. 14 Bwana atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya. 15 Bwana akamwambia Musa, Mbona unanililia mimi? Waambie wana wa Israeli waendelee mbele. 16 Nawe inua fimbo yako, ukanyoshe mkono wako juu ya bahari, na kuigawanya; nao wana wa Israeli watapita kati ya bahari katika nchi kavu. 17 Nami, tazama, nitaifanya mioyo ya Wamisri kuwa migumu, nao wataingia na kuwafuatia, nami nitajipatia utukufu kwa Farao, na kwa jeshi lake lote, kwa magari yake na kwa wapanda farasi wake. 18 Na Wamisri watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapokwisha kujipatia utukufu kwa Farao, na magari yake, na farasi zake. 19 Kisha malaika wa Mungu, aliyetangulia mbele ya jeshi la Israeli, akaondoka akaenda nyuma yao; na ile nguzo ya wingu ikaondoka hapo mbele yao, ikasimama nyuma yao; 20 ikafika kati ya jeshi la Misri na jeshi la Israeli; napo palikuwa na lile wingu na lile giza, lakini lilitoa nuru wakati wa usiku; na hawa hawakuwakaribia hawa usiku kucha. 21 Musa; akanyosha mkono wake juu ya bahari; Bwana akaifanya bahari irudi nyuma kwa upepo wa nguvu utokao mashariki, usiku kucha, akaifanya bahari kuwa nchi kavu, maji yakagawanyika. 22 Wana wa Israeli wakaenda ndani kati ya bahari katika nchi kavu; nayo maji yalikuwa ukuta kwao mkono wa kuume, na mkono wa kushoto. 23 Na wale Wamisri wakawafuatia, wakaingia ndani kati ya bahari, farasi zote za Farao, na magari yake, na wapanda farasi wake. 24 Ikawa katika zamu ya alfajiri, Bwana akalichungulia jeshi la Wamisri katika ile nguzo ya moto na ya wingu, akalifadhaisha jeshi la Wamisri. 25 Akayaondoa magurudumu ya magari yao, hata yakaenda kwa uzito; na Wamisri wakasema, Na tukimbie mbele ya Israeli; kwa kuwa Bwana anawapigania, kinyume cha Wamisri. 26 Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi tena juu ya Wamisri, juu ya magari yao, na juu ya farasi zao. 27 Musa akaunyosha mkono wake juu ya bahari, na kulipopambazuka, bahari ikarudi kwa nguvu zake; Wamisri wakakimbia mbele yake; na Bwana akawakukutia mbali hao Wamisri kati ya bahari. 28 Yale maji yakarudi yakafunikiza magari na wapanda farasi, hata jeshi lote la Farao lililoingia katika bahari nyuma yao; hakusalia hata mtu mmoja. 29 Lakini wana wa Israeli wakaenda katika nchi kavu katikati ya bahari; na hayo maji yalikuwa ni kuta upande wao wa kuume, na upande wao wa kushoto. 30 Ndivyo Bwana alivyowaokoa Israeli siku ile mikononi mwa Wamisri; Waisraeli wakawaona Wamisri ufuoni kwa bahari, wamekufa. 31 Israeli akaiona ile kazi kubwa aliyoifanya Bwana juu ya Wamisri, ndipo hao watu wakamcha Bwana, wakamwamini Bwana, na Musa mtumishi wake.

Kutoka 15

1 Ndipo Musa na wana wa Israeli wakamwimbia Bwana wimbo huu wakanena, na kusema, Nitamwimbia Bwana, kwa maana ametukuka sana; Farasi na mpanda farasi amewatupa baharini. 2 Bwana ni nguvu zangu, na wimbo wangu; Naye amekuwa wokovu wangu. Yeye ni Mungu wangu, nami nitamsifu; Ni Mungu wa baba yangu, nami nitamtukuza. 3 Bwana ni mtu wa vita, Bwana ndilo jina lake. 4 Magari ya Farao na jeshi lake amewatupa baharini, Maakida yake wateule wamezama katika bahari ya Shamu. 5 Vilindi vimewafunikiza, Walizama vilindini kama jiwe. 6 Bwana, mkono wako wa kuume umepata fahari ya uwezo, Bwana, mkono wako wa kuume wawaseta-seta adui. 7 Kwa wingi wa ukuu wako wawaangusha chini wanaokuondokea, Wapeleka hasira yako, nayo huwateketeza kama mabua makavu. 8 Kwa upepo wa mianzi ya pua yako maji yalipandishwa, Mawimbi yakasimama juu wima mfano wa chungu, Vilindi vikagandamana ndani ya moyo wa bahari. 9 Adui akasema, Nitafuatia, nitapata, nitagawanya nyara, Nafsi yangu itashibishwa na wao; Nitaufuta upanga wangu, mkono wangu utawaangamiza. 10 Ulivuma kwa upepo wako, bahari ikawafunikiza; Wakazama kama risasi ndani ya maji makuu. 11 Ee Bwana, katika miungu ni nani aliye kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, Mwenye kuogopwa katika sifa zako, mfanya maajabu? 12 Ulinyosha mkono wako wa kuume, Nchi ikawameza. 13 Wewe kwa rehema zako umewaongoza watu uliowakomboa, Kwa uweza wako uliwaelekeza hata makao yako matakatifu. 14 Kabila za watu wamesikia, wanatetemeka, Wakaao Ufilisti utungu umewashika. 15 Ndipo majumbe wa Edomu wakashangaa, Watu wa Moabu wenye nguvu tetemeko limewapata, Watu wote wakaao Kanaani wameyeyuka. 16 Hofu na woga umewaangukia; Kwa uweza wa mkono wako wanakaa kimya kama jiwe; Hata watakapovuka watu wako, Ee Bwana, Hata watakapovuka watu wako uliowanunua. 17 Utawaingiza, na kuwapanda katika mlima wa urithi wako, Mahali pale ulipojifanyia, Ee Bwana, ili upakae, Pale patakatifu ulipopaweka imara, Bwana, kwa mikono yako. 18 Bwana atatawala milele na milele. 19 Kwa maana farasi za Farao na magari yake na wapanda farasi wake waliingia ndani ya bahari, Bwana akayarudisha maji ya bahari juu yao; bali wana wa Israeli walikwenda katika nchi kavu katikati ya bahari. 20 Na Miriamu, nabii mke, ndugu yake Haruni, akatwaa tari mkononi mwake; wanawake wakatoka wote wakaenda nyuma yake, wenye matari na kucheza. 21 Miriamu akawaitikia,Mwimbieni Bwana ,kwa maana ametukuka sana;Farasi na mpanda farasi amewatupa baharini. 22 Musa akawaongoza Israeli waende mbele kutoka Bahari ya Shamu, nao wakatokea kwa jangwa la Shuri; wakaenda safari ya siku tatu jangwani wasione maji. 23 Walipofika mahali palipoitwa Mara hawakupata kuyanywa yale maji ya Mara, kwa kuwa yalikuwa machungu; kwa ajili ya hayo jina lake likaitwa Mara. 24 Ndipo watu wakamnung'unikia Musa, wakisema, Tunywe nini? 25 Naye akamlilia Bwana; Bwana akamwonyesha mti, naye akautia katika hayo maji, maji yakawa matamu. Basi akawawekea amri na hukumu huko, akawaonja huko; 26 akawaambia, Kwamba utaisikiza kwa bidii sauti ya Bwana, Mungu wako, na kuyafanya yaliyoelekea mbele zake, na kutega masikio usikie maagizo yake, na kuzishika amri zake, mimi sitatia juu yako maradhi yo yote niliyowatia Wamisri; kwa kuwa Mimi ndimi Bwana nikuponyaye. 27 Wakafikilia Elimu, palipokuwa na chemchemi kumi na mbili, na mitende sabini; wakapanga hapo, karibu na maji.

Kutoka 16

1 Kisha wakasafiri kutoka Elimu, na mkutano wote wa wana wa Israeli wakafikilia bara ya Sini, iliyoko kati ya Elimu na Sinai, siku ya kumi na tano ya mwezi wa pili baada ya kutoka kwao nchi ya Misri. 2 Na mkutano mzima wa wana wa Israeli ukawanung'unikia Musa na Haruni, huko barani; 3 wana wa Israeli wakawaambia, Laiti tungalikufa kwa mkono wa Bwana katika nchi ya Misri, hapo tulipoketi karibu na zile sufuria za nyama, tulipokula vyakula hata kushiba; kwani mmetutoa huko na kututia katika bara hii, ili kutuua kwa njaa kusanyiko hili lote. 4 Ndipo Bwana akamwambia Musa, Tazama, mimi nitawanyeshea ninyi mvua ya mkate kutoka mbinguni; na hao watu watatoka nje na kuokota kila siku sehemu ya siku; ili nipate kuwajaribu, kwamba watakwenda katika sheria yangu, ama sivyo. 5 Kisha itakuwa siku ya sita, ya kwamba watayaandaa hayo watakayoleta ndani, nayo yatakuwa ni mara mbili kuliko wayaokotayo kila siku. 6 Musa na Haruni wakawaambia wana wote wa Israeli, Jioni ndipo mtakapojua ya kuwa Bwana amewaleta kutoka nchi ya Misri; 7 na asubuhi ndipo mtakapouona utukufu wa Bwana; kwa kuwa yeye asikia manung'uniko yenu mliyomnung'unikia Bwana; na sisi tu nani, hata mkatunung'unikia? 8 Musa akasema, Ndilo litakalokuwa, hapo Bwana atakapowapa nyama wakati wa jioni mle, na asubuhi mikate hata mkakinai; kwa kuwa Bwana asikia manung'uniko yenu mliyomnung'unikia yeye; na sisi tu nani? Manung'uniko yenu hayakuwa juu yetu sisi, ila juu ya Bwana. 9 Musa akamwambia Haruni, Haya, sema na mkutano wote wa wana wa Israeli, Njoni karibu mbele ya Bwana; kwa kuwa yeye ameyasikia manung'uniko yenu. 10 Ilikuwa Haruni aliponena na huo mkutano wote wa wana wa Israeli, wakaangalia upande wa bara, na tazama, utukufu wa Bwana ukaonekana katika hilo wingu. 11 Bwana akasema na Musa, akinena, 12 Nimeyasikia manung'uniko ya wana wa Israeli; haya sema nao, ukinena, Wakati wa jioni mtakula nyama, na wakati wa asubuhi mtashiba mkate; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 13 Ikawa wakati wa jioni, kware wakakaribia, wakakifunikiza kituo; na wakati wa asubuhi umande ulikuwa juu ya nchi pande zote za kituo. 14 Na ulipoinuka ule umande uliokuwa juu ya nchi, kumbe! Juu ya uso wa bara kitu kidogo kilichoviringana, kidogo kama sakitu juu ya nchi. 15 Wana wa Israeli walipokiona, wakaambiana, Nini hiki? Maana hawakujua ni kitu gani. Musa akawaambia, Ndio mkate ambao Bwana amewapa ninyi, mle. 16 Neno hili ndilo aliloagiza Bwana, Okoteni ninyi kitu hicho kila mtu kama ulaji wake ulivyo; kichwa pishi,kama hesabu ya watu wenu ilivyo ;ndivyo mtakavyotwaa,kila mtu kwa ajili ya hao walioko hemani mwake. 17 Wana wa Israeli wakafanya hivyo, wakaokota wengine zaidi, wengine kupungua. 18 Nao walipoipima kwa pishi, yeye aliyekuwa ameokota kingi hakubakiwa na kitu, na yeye aliyekuwa ameokota kichache hakupungukiwa; wakaokota kila mtu kama ulaji wake ulivyokuwa. 19 Musa akawaambia, Mtu awaye yote asikisaze hata asubuhi. 20 Lakini hawakumsikiza Musa; wengine miongoni mwao wakakisaza hata asubuhi, nacho kikaingia mabuu na kutoa uvundo; Musa akawakasirikia sana. 21 Basi wakaokota asubuhi baada ya asubuhi, kila mtu kama ulaji wake ulivyokuwa; na hapo jua lilipokuwa ni kali, kikayeyuka. 22 Basi ikawa siku ya sita wakaokota kile chakula sehemu maradufu, kila mtu pishi mbili; na wazee wote wa mkutano wakaenda na kumwambia Musa. 23 Akawaambia, Ndilo neno alilonena Bwana Kesho ni starehe takatifu, Sabato takatifu kwa Bwana; okeni mtakachooka, na kutokosa mtakachotokosa; na hicho kitakachowasalia jiwekeeni kilindwe hata asubuhi. 24 Basi wakakiweka hata asubuhi, kama Musa alivyowaagiza; nacho hakikutoa uvundo wala kuingia mabuu. 25 Musa akasema, Haya, kuleni hiki leo; kwa kuwa leo ni Sabato ya Bwana; leo hamtakiona nje barani. 26 Siku sita mtaokota; lakini siku ya saba ni Sabato, siku hiyo hakitapatikana. 27 Ikawa siku ya saba wengine wakatoka kwenda kukiokota, wasikione. 28 Bwana akamwambia Musa, Mtakataa kuyashika maagizo yangu na sheria zangu hata lini? 29 Angalieni, kwa kuwa Bwana amewapa ninyi hiyo Sabato, kwa sababu hii huwapa siku ya sita chakula cha siku mbili; kaeni kila mtu mahali pake, mtu awaye yote asiondoke mahali pake kwa siku ya saba. 30 Basi hao watu wakapumzika kwa siku ya saba. 31 Na nyumba ya Israeli wakakiita jina lake Mana; nacho kilikuwa mfano wa chembe za mtama, nyeupe; na tamu yake ilikuwa kama tamu ya maandazi membamba yaliyoandaliwa kwa asali. 32 Musa akasema, Hili ni neno Bwana aliloliamuru, Pishi moja ya kitu hicho na kiwekwe kwa ajili ya vizazi vyenu; ili kwamba wao wapate kukiona kile chakula nilichowalisha ninyi barani, hapo nilipowaleta kutoka nchi ya Misri. 33 Basi Musa akamwambia Haruni, Twaa kopo, ukatie pishi moja ya hiyo Mana ndani yake, uiweke mbele ya Bwana, ilindwe kwa ajili ya vizazi vyenu. 34 Kama vile Bwana alivyomwagizia Musa ndivyo Haruni alivyoiweka hapo mbele ya Ushahidi, ili ilindwe. 35 Na wana wa Israeli walikula Mana muda wa miaka arobaini, hata walipofikilia nchi iliyo na watu, wakala ile Mana, hata walipofikilia mipakani mwa nchi ya Kanaani. 36 Hiyo omeri ni sehemu kumi ya efa.

Kutoka 17

1 Mkutano wote wa wana wa Israeli ukasafiri, kutoka bara ya Sini kwa safari zao, kama Bwana alivyowaagiza, wakatua Refidimu; napo hapakuwa na maji, watu wanywe. 2 Kwa hiyo hao watu wakateta na Musa, wakasema, Tupe maji tunywe. Musa akawaambia, Kwani kuteta na mimi? Mbona mnamjaribu Bwana? 3 Watu wakawa na kiu huko; nao wakamnung'unikia Musa, wakasema, Mbona umetupandisha kutoka Misri, kutuua sisi na watoto wetu na wanyama wetu kwa kiu? 4 Musa akamlilia Bwana, akisema, Niwatendee nini watu hawa? Bado kidogo nao watanipiga kwa mawe. 5 Bwana akamwambia Musa, Pita mbele ya watu, ukawachukue baadhi ya wazee wa Israeli pamoja nawe; na ile fimbo yako ambayo uliupiga mto kwayo, uitwae mkononi mwako, ukaende. 6 Tazama, nitasimama mbele yako huko, juu ya lile jabali katika Horebu; nawe utalipiga jabali, na maji yatatoka, watu wapate kunywa. Musa akafanya hivyo mbele ya wazee wa Israeli. 7 Akapaita mahali pale jina lake Masa, na Meriba; kwa sababu ya mateto ya wana wa Israeli, na kwa sababu walimjaribu Bwana, wakisema, Je! Bwana yu kati yetu au sivyo? 8 Wakati huo Waamaleki wakatokea, wakapigana na Israeli huko Refidimu. 9 Musa akamwambia Yoshua, Tuchagulie watu, ukatoke upigane na Waamaleki; kesho nitasimama juu ya kilele kile, na ile fimbo ya Mungu nitakuwa nayo mkononi mwangu. 10 Basi Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia, akapigana na Amaleki; na Musa na Haruni na Huri wakapanda juu ya kile kilima. 11 Ikawa, Musa alipouinua mkono wake, Israeli walishinda; na alipoushusha mkono wake, Amaleki walishinda. 12 Lakini mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa. 13 Yoshua akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga. 14 Bwana akamwambia Musa, Andika habari hii katika kitabu iwe ukumbusho, kisha ihubiri masikioni mwa Yoshua; ya kuwa nitaufuta ukumbusho wa Amaleki kabisa, usiwe tena chini ya mbingu. 15 Musa akajenga madhabahu, akaiita jina lake Yehova-nisi; 16 akasema, Bwana ameapa; Bwana atakuwa na vita na Amaleki kizazi baada ya kizazi.

Kutoka 18

1 Basi Yethro, kuhani wa Midiani, mkwewe Musa, alisikia habari ya mambo hayo yote Mungu aliyokuwa amemtendea Musa, na Waisraeli watu wake, jinsi Bwana alivyowaleta Israeli watoke Misri. 2 Ndipo Yethro mkwewe Musa akamtwaa Sipora, mke wa Musa, baada ya yeye kumrudisha, 3 pamoja na wanawe wawili; katika hao, jina la mmoja ni Gershomu, maana alisema, Mimi nimekuwa mgeni katika nchi ya ugenini; 4 na jina la wa pili ni Eliezeri, kwa kuwa alisema, Yeye Mungu wa baba yangu alikuwa msaada wangu, akaniokoa na upanga wa Farao. 5 Basi Yethro, mkwewe Musa, pamoja na mke wa Musa na wanawe wawili wakamwendea Musa huko nyikani, hapo alipokuwa amepanga, kwenye mlima wa Mungu; 6 naye akamwambia Musa, Mimi Yethro mkweo nimekuja kwako, na mkeo, na wanawe wawili pamoja naye. 7 Basi Musa akatoka nje ili amlaki mkwewe, akasujudia na kumbusu; nao wakaulizana habari; kisha wakaingia hemani. 8 Musa akamwambia mkwewe mambo hayo yote Bwana aliyomtenda Farao na Wamisri kwa ajili ya Israeli, na mambo mazito yote yaliyowapata njiani, na jinsi Bwana alivyowaokoa. 9 Yethro alifurahi kwa ajili ya wema wote Bwana aliowatendea Israeli, kwa alivyo waokoa mikononi mwa Wamisri. 10 Kisha Yethro akasema, Na ahimidiwe Bwana aliyewaokoa na mikono ya Wamisri, na mkono wa Farao; aliyewaokoa watu hao watoke mikononi mwa Wamisri. 11 Sasa najua ya kuwa Bwana ni mkuu kuliko miungu yote; naam, katika jambo hilo walilowatenda kwa unyeti. 12 Yethro mkwewe Musa akamletea Mungu sadaka ya kuteketezwa na dhabihu; na Haruni akaja, na wazee wote wa Israeli, wale chakula pamoja na mkwewe Musa mbele za Mungu. 13 Asubuhi yake Musa akaketi ili awapishie hukumu watu; na hao watu wakasimama kumzunguka Musa tangu asubuhi hata jioni. 14 Mkwewe Musa alipoyaona yote aliyowafanyia watu, akasema, Ni jambo gani hili uwatendealo hao watu? Kwani wewe kuketi hapo peke yako, na watu wote kusimama kwako tangu asubuhi hata jioni? 15 Musa akamwambia mkwewe, Ni kwa sababu watu hunijilia mimi wapate kumwuliza Mungu; 16 wakiwa na neno, hunijilia; nami naamua kati ya mtu na mwenziwe, nami nawajuvisha amri za Mungu, na sheria zake. 17 Mkwewe Musa akamwambia, Jambo hili ufanyalo si jema. 18 Huna budi utadhoofika wewe, na hawa watu walio pamoja nawe pia; maana jambo hili ni zito mno kwako; huwezi wewe kulitenda peke yako. 19 Sikiza sasa neno langu, nitakupa shauri, na Mungu na awe pamoja nawe; uwe wewe kwa ajili ya watu mbele ya Mungu, nawe umletee Mungu maneno yao; 20 nawe utawafundisha zile amri na sheria, nawe utawaonyesha njia ambayo inawapasa kuiendea, na kazi ambayo inawapasa kuifanya. 21 Zaidi ya hayo utajipatia katika watu hawa watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu; ukawaweka juu yao, wawe wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini, na wakuu wa kumi; 22 nao wawaamue watu hawa sikuzote; kisha, kila neno lililo kubwa watakuletea wewe, lakini kila neno dogo wataliamua wenyewe; basi kwako wewe mwenyewe utapata nafasi zaidi, nao watauchukua huo mzigo pamoja nawe. 23 Kwamba utafanya jambo hili, na Mungu akikuagiza hivyo, basi utaweza kusimama wewe, na watu hawa wote nao watakwenda mahali pao kwa amani. 24 Basi Musa akasikiza neno la mkwewe, akayafanya yote aliyokuwa amemwambia. 25 Musa akawachagua watu wenye uwezo katika Israeli yote, akawaweka wawe vichwa juu ya watu, wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini, na wakuu wa kumi. 26 Nao wakawaamua watu sikuzote; mashauri magumu wakamletea Musa, lakini kila neno dogo wakaliamua wenyewe. 27 Kisha Musa akaagana na mkwewe; naye akaenda zake, mpaka nchi yake mwenyewe.

Kutoka 19

1 Mwezi wa tatu baada ya kutoka Waisraeli katika nchi ya Misri, siku iyo hiyo wakafika jangwa la Sinai. 2 Nao walipokuwa wameondoka Refidimu na kufika jangwa la Sinai, wakatua katika lile jangwa; Israeli wakapiga kambi huko wakiukabili mlima. 3 Musa akapanda kwa Mungu, na Bwana akamwita toka mlima ule, akisema, Utawaambia nyumba ya Yakobo, na kuwaarifu wana wa Israeli, maneno haya; 4 Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi. 5 Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, 6 nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu. Hayo ndiyo maneno utakayowaambia wana wa Israeli. 7 Musa akaenda akawaita wazee wa watu, akawafunulia maneno hayo yote, Bwana aliyokuwa amemwagiza. 8 Watu wote wakaitika pamoja wakisema, Hayo yote aliyoyasema Bwana tutayatenda. Naye Musa akamwambia Bwana maneno ya hao watu. 9 Bwana akamwambia Musa, Tazama, mimi naja kwako katika wingu zito ili watu hawa wasikie nitakaposema nawe, nao wapate kukuamini wewe nawe hata milele. Musa akamwambia Bwana hayo maneno ya watu. 10 Bwana akamwambia Musa, Enenda kwa watu hawa, ukawatakase leo na kesho, wakazifue nguo zao, 11 wawe tayari kwa siku ya tatu; maana siku ya tatu Bwana atashuka katika mlima wa Sinai machoni pa watu hawa wote. 12 Nawe utawawekea mipaka watu hawa pande zote, ukisema, Jihadharini, msipande mlima huu, wala msiuguse, hata mapambizo yake; kila mtu atakayeugusa mlima huu, bila shaka atauawa. 13 Mkono wa mtu awaye yote usimguse mtu huyo, ila hakika yake atapigwa kwa mawe, au kupigwa kwa mkuki; kwamba ni mnyama au kwamba ni mwanadamu, hataishi. Hapo panda itakapotoa sauti kwa kufuliza ndipo watakapoukaribia mlima. 14 Musa akatelemka mlimani akawaendea watu akawatakasa, nao wakafua nguo zao. 15 Akawaambia watu; Mwe tayari siku ya tatu; msimkaribie mwanamke. 16 Ikawa siku ya tatu, wakati wa asubuhi, palikuwa na ngurumo na umeme, na wingu zito juu ya mlima, na sauti ya baragumu iliyolia sana. Watu wote waliokuwa kituoni wakatetemeka. 17 Musa akawatoa hao watu katika kituo, akawaleta ili waonane na Mungu; wakasimama pande za chini za kile kilima. 18 Mlima wa Sinai wote pia ukatoa moshi, kwa sababu Bwana alishuka katika moto; na ule moshi wake ukapanda juu kama moshi wa tanuu, mlima wote ukatetemeka sana. 19 Na hapo sauti ya baragumu ilipozidi kulia sana, Musa akanena, naye Mungu akamwitikia kwa sauti. 20 Bwana akaushukia mlima, juu ya kilele cha mlima; Bwana akamwita Musa aende hata kilele cha mlima; Musa akapanda juu. 21 Ndipo Bwana akamwambia Musa, Shuka chini, uwaonye watu wasije wakapasua njia waje kwa Bwana kutazama, kisha wengi miongoni mwao wakaangamia. 22 Makuhani nao, wamkaribiao Bwana, na wajitakase, Bwana asije akawafurikia. 23 Musa akamwambia Bwana, Watu hawa hawawezi kuukaribia mlima wa Sinai; kwa kuwa wewe ulituusia, ukisema, Wekeni mipaka kando-kando ya mlima, na kuutenga. 24 Bwana akamwambia, Nenda, ushuke wewe; nawe utakwea, wewe, na Haruni pamoja nawe; lakini wale makuhani na watu wasipenye kumkaribia Bwana, asije yeye akawafurikia juu yao. 25 Basi Musa akawatelemkia hao watu na kuwaambia hayo.

Kutoka 20

1 Mungu akanena maneno haya yote akasema, 2 Mimi ni Bwana, Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa. 3 Usiwe na miungu mingine ila mimi. 4 Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. 5 Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao, 6 nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu. 7 Usilitaje bure jina la Bwana, Mungu wako, maana Bwana hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure. 8 Ikumbuke siku ya Sabato uitakase. 9 Siku sita fanya kazi, utende mambo yako yote; 10 lakini siku ya saba ni Sabato ya Bwana, Mungu wako, siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala mnyama wako wa kufuga, wala mgeni aliye ndani ya malango yako. 11 Maana, kwa siku sita Bwana alifanya mbingu, na nchi, na bahari, na vyote vilivyomo, akastarehe siku ya saba; kwa hiyo Bwana akaibarikia siku ya Sabato akaitakasa. 12 Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako. 13 Usiue. 14 Usizini. 15 Usiibe. 16 Usimshuhudie jirani yako uongo. 17 Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng'ombe wake, wala punda wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako. 18 Watu wote wakaona umeme na ngurumo na sauti ya baragumu, na ule mlima kutoka moshi; na watu walipoona hayo wakatetemeka, wakasimama mbali. 19 Wakamwambia Musa, Sema nasi wewe, nasi tutasikia, bali Mungu asiseme nasi, tusije tukafa. 20 Musa akawaambia watu, Msiogope, maana Mungu amekuja ili awajaribu, na utisho wake uwe mbele yenu, ili kwamba msifanye dhambi. 21 Basi hao watu wakasimama mbali, naye Musa akalikaribia lile giza kuu Mungu alipokuwapo. 22 Bwana akamwambia Musa, Waambie wana wa Israeli hivi, Ninyi wenyewe mmeona ya kuwa nimenena nanyi kutoka mbinguni. 23 Msifanye miungu mingine pamoja nami; miungu ya fedha, wala miungu ya dhahabu, msijifanyie. 24 Utanifanyia madhabahu ya udongo, nawe utatoa dhabihu zako juu yake; sadaka za kuteketezwa, na sadaka za amani, kondoo zako, na ng'ombe zako, kila mahali nitakapotia ukumbusho wa jina langu, hapo ndipo nitakapokujilia na kukubarikia. 25 Nawe ukinifanyia madhabahu ya mawe, hutaijenga ya mawe yaliyochongwa; kwa kuwa ukiwa wewe umetumia chombo chako katika kuichonga umeitia unajisi. 26 Tena hutapanda kwenda madhabahuni kwangu kwa daraja, uchi wako usidhihirike juu yake.

Kutoka 21

1 Basi hukumu utakazoziweka mbele ya watu ni hizi 2 Ukimnunua mtumwa wa Kiebrania, atakutumikia muda wa miaka sita; mwaka wa saba atatoka kwako huru bure. 3 Kwamba aliingia kwako peke yake tu, atatoka hivyo peke yake; kwamba ameoa, mkewe atatoka aende pamoja naye. 4 Kwamba ni bwana wake aliyempa huyo mke, naye amemzalia wana, wa kiume au wa kike; yule mke na wanawe watakuwa ni mali ya bwana wake, naye mume atatoka peke yake. 5 Lakini huyo mtumwa akisema waziwazi, Mimi nampenda bwana wangu, na mke wangu na watoto wangu; sitaki mimi kutoka niwe huru; 6 ndipo hapo huyo bwana wake atamleta mbele ya Mungu na kumleta mlangoni, au penye mwimo wa mlango; na bwana wake atalitoboa sikio lake kwa uma; ndipo atamtumikia sikuzote. 7 Mtu akimwuza binti yake awe kijakazi, hatatoka yeye kama watumwa wa kiume watokavyo. 8 Kwamba bwana wake hakupendezewa naye, akiwa amemposa, ndipo atakubali akombolewe; hana amri yeye kumwuza aende kwa watu wageni maana amemtenda kwa udanganyifu. 9 Kwamba amposa mwanawe, atamtendea kama desturi zipasazo binti zake. 10 Kwamba ajitwalia mke mwingine, chakula chake huyo, na nguo zake, na ngono yake, hatampunguzia. 11 Kwamba hamfanyii mambo haya matatu, ndipo atatoka aende bure, pasipo kutolewa mali. 12 Mtu awaye yote ampigaye mtu, hata akafa, hana budi atauawa huyo. 13 Lakini kama hakumvizia, ila Mungu amemtia mkononi mwake; basi nitakuonyesha mahali atakapopakimbilia. 14 Lakini, mtu akimwendea mwenziwe kwa kujikinai, kusudi apate kumwua kwa hila; huyo utamwondoa hata madhabahuni pangu, auawe. 15 Ampigaye baba yake au mama yake, sharti atauawa. 16 Yeye amwibaye mtu, na kumwuza, au akipatikana mkononi mwake, sharti atauawa huyo 17 Yeye amwapizaye baba yake au mama yake, sharti atauawa. 18 Watu wakigombana, na mmoja akimpiga mwenziwe kwa jiwe, au kwa konde, asife, lakini yualazwa kitandani mwake; 19 atakapoinuka tena na kuenenda nje kwa kutegemea fimbo, ndipo hapo yule aliyempiga ataachwa; ila atamlipa kwa ajili ya hayo majira yake yaliyompotea, naye atamwuguza hata apone kabisa. 20 Mtu akimpiga mtumwa wake, au kijakazi chake, kwa fimbo, naye akifa mkononi mwake, hana budi ataadhibiwa. 21 Lakini akipona siku moja au mbili hataadhibiwa; maana, ni mali yake. 22 Watu waume wakiteta pamoja, wakamwumiza mwanamke mwenye mimba hata akaharibu mimba, tena yasiwe madhara zaidi; sharti atatozwa mali kama atakavyomwandikia mumewe huyo mwanamke; atalipa kama hao waamuzi watakavyosema. 23 Lakini kwamba pana madhara zaidi, ndipo utatoza uhai kwa uhai, 24 jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu, 25 kuteketeza kwa kuteketeza, jeraha kwa jeraha, chubuko kwa ajili ya chubuko. 26 Mtu akimpiga mtumwa wake jicho, au jicho la kijakazi chake, na kuliharibu; atamwacha huru kwa ajili ya jicho lake. 27 Au akimpiga mtumwa wake jino likang'oka, au jino la kijakazi chake, atamwacha huru kwa ajili ya jino lake. 28 Ng'ombe akipiga pembe mtu mume au mtu mke, nao wakafa, huyo ng'ombe atauawa kwa kupigwa kwa mawe, nyama yake isiliwe; lakini mwenye huyo ng'ombe ataachiliwa. 29 Lakini kwamba huyo ng'ombe alizoea kupiga watu tangu hapo, naye mwenyewe ameonyeshwa jambo hilo, wala asimzuie, naye amemwua mtu mume au mwanamke; huyo ng'ombe atauawa kwa kupigwa kwa mawe, na huyo mwenyewe naye atauawa. 30 Lakini akiandikiwa ukombozi, ndipo atakapotoa kwa ajili ya uhai wake hicho atakachoandikiwa. 31 Akiwa ng'ombe amempiga pembe mtoto wa kiume na kumtumbua, au akiwa amempiga mtoto wa kike, atatendwa kama hukumu hiyo. 32 Ng'ombe akimtumbua mtumwa mume au kijakazi; mwenye ng'ombe atampa bwana wao shekeli thelathini za fedha, naye ng'ombe atauawa kwa kupigwa kwa mawe. 33 Kwamba mtu atafunua shimo, au kuchimba shimo, naye asilifunike, kisha ikawa ng'ombe au punda kutumbukia humo, 34 mwenye shimo atalipa; atampa huyo mwenye mnyama fedha, na mnyama aliyekufa atakuwa ni wake. 35 Ng'ombe wa mtu akimwumiza ng'ombe wa mtu mwingine hata akafa; ndipo watamwuza huyo ng'ombe aliye hai na kugawanya thamani yake; na ng'ombe aliyekufa pia watamgawanya. 36 Au kwamba ilijulikana ya kuwa ng'ombe tangu hapo amezoea kupiga kwa pembe, wala mwenyewe asimzuie; ndipo atakapolipa yeye, ng'ombe kwa ng'ombe, na huyo ng'ombe aliyekufa atakuwa ni wake.

Kutoka 22

1 Mtu akiiba ng'ombe au kondoo, na kumchinja, au kumwuza; atalipa ng'ombe watano badala ya ng'ombe mmoja, na kondoo wanne badala ya kondoo mmoja. 2 Mwivi akipatikana akiwa yu hali ya kuvunja mahali, naye akapigwa hata akafa, hapatakuwa na malipizo ya damu kwa ajili yake. 3 Lakini kama jua limekucha juu yake, ndipo patakuwa na malipizo ya damu kwa ajili yake; ingempasa kutoa malipo kamili; akiwa hana kitu, na auzwe kwa ajili ya wivi wake. 4 Kama hicho kitu kilichoibwa chapatikana hai mkononi mwake, kama ni ng'ombe, au punda, au kondoo; atalipa thamani yake mara mbili. 5 Mtu akilisha katika shamba, au shamba la mizabibu, akimwacha mnyama wake, akala katika shamba la mtu mwingine; atalipa katika vitu vilivyo vizuri vya shamba lake mwenyewe, au vya mizabibu yake. 6 Ukiwaka moto, na kushika penye miiba, na ngano zilizofungwa miganda, au ngano ambazo hazijakatwa, au shamba, likateketea; yeye aliyeuwasha huo moto lazima atalipa. 7 Mtu akimpa mwenziwe amana ya fedha au vitu vingine amtunzie, na vitu vile vikaibwa katika nyumba ya mtu huyo; mwivi akipatikana, atalipa thamani yake mara mbili. 8 Mwivi asipopatikana, ndipo mwenye nyumba atakaribia mbele ya Mungu, ionekane kwamba si yeye aliyetia mkono na kutwaa vyombo vya mwenziwe. 9 Kila jambo la kukosana, kama ni la ng'ombe, au la punda, au la kondoo, au la mavazi, au la kitu cho chote kilichopotea, ambacho mtu mmoja asema ni chake, hilo jambo la watu wote wawili litaletwa mbele ya Mungu; na yeye atakayehukumiwa na Mungu kuwa ni mkosa atamlipa mwenziwe thamani yake mara mbili. 10 Mtu akimpa mwenziwe punda, au ng'ombe, au kondoo, au mnyama ye yote, ili amtunzie; yule mnyama akafa, au akaumia, au akachukuliwa mtu asione; 11 patakuwa na kiapo cha Bwana katikati ya watu hao wawili, kwamba alipeleka mkono wake kutwaa mali ya mwenziwe, na mwenyewe atakubali hayo, wala hatalipa. 12 Lakini kwamba aliibiwa mnyama huyo, sharti amlipe yule mwenyewe. 13 Kwamba aliraruliwa na mnyama mkali, na amlete uwe ushahidi; hatalipa kwa ajili ya mnyama aliyeraruliwa. 14 Mtu akiazima mnyama kwa mwenziwe, naye akaumia huyo mnyama, au akafa, mwenyewe asipokuwapo, lazima atalipa. 15 Kama huyo mwenyewe alikuwapo pamoja na mnyama wake, hatalipa; kama ni mnyama aliyeajiriwa, alikwenda kwa ajili ya ujira wake. 16 Mtu akimshawishi mwanamwali, aliyeposwa na mume, na kulala naye, lazima atatoa mahari kwa ajili yake ili awe mkewe. 17 Ikiwa baba yake huyo mwanamwali akataa kabisa kumpa, atalipa fedha kama hesabu ya mahari ya mwanamwali ilivyo. 18 Usimwache mwanamke mchawi kuishi. 19 Mtu awaye yote alalaye na mnyama sharti atauawa. 20 Mtu atakayemchinjia sadaka mungu ye yote, isipokuwa ni yeye Bwana peke yake, na angamizwe kabisa. 21 Usimwonee mgeni, wala kumtendea jeuri; kwa kuwa ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri. 22 Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima. 23 Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao, 24 na hasira yangu itawaka moto, nami nitawaua ninyi kwa upanga; na wake wenu watakuwa wajane, na watoto wenu mayatima. 25 Ukimkopesha mtu aliye maskini, katika watu wangu walio pamoja nawe; usiwe kwake mfano wa mwenye kumdai; wala hutamwandikia faida. 26 Ikiwa wewe kwa njia yo yote wapokea nguo ya jirani yako rehani, lazima utamrudishia mbele ya jua kuchwa; 27 maana hiyo nguo ni kifuniko chake, hiyo peke yake ni nguo ya ngozi yake; je! Atalalia nini? Itakuwa, hapo atakaponililia mimi, nitasikia; kwa kuwa mimi ni mwenye rehema. 28 Usimtukane Mungu, wala usimlaani mkuu wa watu wako. 29 Usikawie kuleta malimbuko ya matunda yako na ya vinywaji vyako. Mzaliwa wa kwanza katika wanao waume utanipa mimi. 30 Nawe utafanya vivyo katika ng'ombe zako, na kondoo zako; utamwacha siku saba pamoja na mama yake; siku ya nane utanipa mimi. 31 Nanyi mtakuwa watu watakatifu kwangu mimi; kwa hiyo msiile nyama yo yote iliyoraruliwa huko kondeni na mnyama wa mwitu; mtawatupia mbwa nyama hiyo.

Kutoka 23

1 Usivumishe habari za uongo; usitie mkono wako pamoja na mwovu, kuwa shahidi wa udhalimu. 2 Usiandamane na mkutano kutenda uovu; wala usitie ushahidi wako katika neno lo lote kwa kugeukia kando na kuandamana na mkutano ili kupotoa hukumu; 3 wala usimpendelee mtu mnyonge katika neno lake. 4 Ukimwona ng'ombe wa adui wako, au punda wake, amepotea, sharti umrudishie mwenyewe tena. 5 Ukimwona punda wake huyo akuchukiaye hali ameanguka chini ya mzigo wake, nawe ungejizuia usimsaidie, lazima umsaidie. 6 Usipotoe hukumu ya mtu maskini katika neno lake. 7 Jitenge mbali na neno uongo; wala wasio hatia na wenye haki usiwaue; kwa kuwa mimi sitamhesabia haki yeye aliye mwovu. 8 Nawe usipokee rushwa; kwani hiyo rushwa huwapofusha macho hao waonao, na kuyapotoa maneno ya wenye haki. 9 Usimwonee mgeni; maana, ninyi mwajua moyo wa mgeni ulivyo, kwa kuwa ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri. 10 Utapanda mbegu katika nchi yako muda wa miaka sita na kuyavuna maongeo yake; 11 lakini mwaka wa saba utaiacha nchi ipumzike na kutulia; hao maskini miongoni mwa watu wako wapate kula; na hicho watakachosaza wao, wapate kula wanyama wa kondeni. Utafanya vivyo katika shamba lako la mizabibu, na katika shamba lako la mizeituni. 12 Siku sita utafanya kazi yako, na siku ya saba utapumzika; ili kwamba ng'ombe wako na punda wako wapate kupumzika, kisha mwana wa mjakazi wako na mgeni wapate kuburudika. 13 Yaangalieni hayo yote niliyowaambia; wala msitaje kabisa majina ya miungu mingine, wala yasisikizwe kutoka kinywani mwako. 14 Mara tatu kila mwaka utaniwekea sikukuu. 15 Utaiweka sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu; utakula mikate isiyochachwa muda wa siku saba kama nilivyokuagiza, kwa wakati uliowekwa, mwezi wa Abibu (kwa maana ndio mwezi uliotoka Misri); wala hapana mtu atakayeonekana mbele yangu na mikono mitupu; 16 tena, sikukuu ya mavuno, hayo malimbuko ya kazi zako za kupanda mashambani; tena, sikukuu ya kukusanya, mwisho wa mwaka, hapo utakapokusanya hayo uliyoyataabikia shambani. 17 Mara tatu katika mwaka watu waume wako wote watahudhuria mbele ya Bwana MUNGU. 18 Usisongeze damu ya dhabihu zangu pamoja na mkate uliotiwa chachu, wala mafuta ya sikukuu yangu usiyaache kusalia hata asubuhi. 19 Ya kwanza ya malimbuko ya nchi yako utayaleta na kuyatia ndani ya nyumba ya Bwana, Mungu wako. Usimtokose mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake. 20 Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea. 21 Jitunzeni mbele yake, mwisikize sauti yake; wala msimtie kasirani; maana, hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa jina langu limo ndani yake. 22 Lakini ukiisikiza sauti yake kweli, na kuyatenda yote ninenayo mimi; ndipo mimi nitakuwa ni adui wa adui zako, na mtesi wa hao wakutesao. 23 Kwa kuwa malaika wangu atatangulia mbele yako, na kukufikisha kwenye Mwamori, na Mhiti, na Mperizi, na Mkanaani, na Mhivi, na Myebusi; nami nitawakatilia mbali. 24 Usiisujudie miungu yao, wala kuitumikia; wala usitende mfano wa matendo yao; bali utaiangamiza kabisa, na nguzo zao utazivunja vipande vipande. 25 Nanyi mtamtumikia Bwana, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. 26 Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza. 27 Nitatuma utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao. 28 Nami nitapeleka mavu mbele yako, watakaomfukuza Mhivi, na Mkanaani, na Mhiti, watoke mbele yako. 29 Sitawafukuza mbele yako katika mwaka mmoja; nchi isiwe ukiwa, na wanyama wa bara wakaongezeka kukusumbua. 30 Nitawafukuza kidogo kidogo mbele yako, hata utakapoongezeka wewe, na kuirithi hiyo nchi. 31 Nami nitakuwekea mpaka wako tangu Bahari ya Shamu hata bahari ya Wafilisti, tena tangu jangwani hata huo Mto; kwa kuwa nitawatia wenyeji wa nchi mkononi mwako; nawe utawafukuza mbele yako. 32 Usifanye maagano pamoja nao, wala pamoja na miungu yao. 33 Wasikae katika nchi yako, wasije wakakufanya kunitendea mimi dhambi; kwa sababu ukiitumikia miungu yao, jambo hili halikosi litakuwa ni tanzi kwako.

Kutoka 24

1 Kisha Bwana akamwambia Musa, Kweeni wewe, na Haruni, na Nadabu, na Abihu, na watu sabini wa wazee wa Israeli, mkamfikilie Bwana; mkasujudie kwa mbali; 2 na Musa peke yake ndiye atakayekaribia karibu na Bwana; lakini hao hawatakaribia karibu; wala hao watu hawatakwea pamoja naye. 3 Musa akaenda akawaambia watu maneno yote ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda. 4 Basi Musa akayaandika maneno yote ya Bwana, akaondoka asubuhi na mapema, akajenga madhabahu chini ya mlima, na nguzo kumi na mbili, kwa hesabu ya kabila kumi na mbili za Israeli, 5 akapeleka vijana wa wana wa Israeli, waliotoa sadaka za kuteketezwa, wakamchinjia Bwana sadaka za amani za ng'ombe. 6 Musa akatwaa nusu ya ile damu, akaitia katika mabakuli; na nusu ya ile damu akainyunyiza juu ya madhabahu. 7 Kisha akakitwaa kitabu cha agano akakisoma masikioni mwa watu; wakasema, Hayo yote aliyoyanena Bwana tutayatenda, nasi tutatii. 8 Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana pamoja nanyi katika maneno haya yote. 9 Ndipo akakwea juu, Musa, na haruni, na Nadabu, na Abihu, na watu sabini miongoni mwa wazee wa Israeli; 10 wakamwona Mungu wa Israeli; chini ya miguu yake palikuwa na kama sakafu iliyofanyizwa kwa yakuti samawi, kama zile mbingu zenyewe kwa usafi wake. 11 Naye hakuweka mkono wake juu ya hao wakuu wa wana wa Israeli; nao wakamwona Mungu, wakala na kunywa. 12 Bwana akamwambia Musa, Njoo huku juu kwangu mlimani, uwe huku; nami nitakupa mbao za mawe na ile sheria na hiyo amri niliyoiandika ili uwafundishe. 13 Musa akaondoka na Yoshua, mtumishi wake, Musa akapanda mlimani kwa Mungu. 14 Akawaambia hao wazee, Tungojeeni hapa, mpaka tutakaporudi kwenu; na tazameni, Haruni na Huri wapo pamoja nanyi; kila mtu aliye na neno na awaendee. 15 Musa akapanda mlimani, lile wingu likaufunikiza mlima. 16 Na huo utukufu wa Bwana ukakaa juu ya mlima wa Sinai; lile wingu likaufunikiza siku sita; na siku ya saba akamwita Musa toka kati ya lile wingu. 17 Na kuonekana kwake ule utukufu wa Bwana kulikuwa kama moto uteketezao, juu ya mlima machoni pa wana wa Israeli. 18 Musa akaingia ndani ya lile wingu, akapanda mlimani; Musa akawa humo katika ule mlima siku arobaini, mchana na usiku.

Kutoka 25

1 Bwana akanena na Musa, akamwambia, 2 Waambie wana wa Israeli kwamba wanitwalie sadaka; kila mtu ambaye moyo wake wampa kupenda mtatwaa kwake sadaka yangu. 3 Sadaka utakayopokea mikononi mwao ni hii; dhahabu, na fedha, na shaba, 4 na nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na nguo za kitani safi, na singa za mbuzi; 5 na ngozi za kondoo waume zilizotiwa rangi nyekundu, na ngozi za pomboo, na miti ya mshita, 6 na mafuta ya ile taa, na viungo vya manukato kwa yale mafuta ya kupaka, na kwa ule uvumba wenye harufu nzuri; 7 na vito vya shohamu, na vito vingine vya kutiwa kwa ile naivera, na kwa kile kifuko cha kifuani. 8 Nao na wanifanyie patakatifu; ili nipate kukaa kati yao. 9 Sawasawa na haya yote nikuonyeshayo, mfano wa maskani, na mfano wa vyombo vyake vyote, ndivyo mtakavyovifanya. 10 Nao na wafanye sanduku la mti wa mshita; urefu wake na uwe dhiraa mbili na nusu, na upana wake dhiraa moja na nusu, na kwenda juu kwake dhiraa moja na nusu. 11 Nawe ulifunike kwa dhahabu safi, ulifunike ndani na nje, nawe tia na ukingo wa dhahabu kulizunguka pande zote. 12 Nawe subu vikuku vinne vya dhahabu kwa ajili yake, na kuvitia katika miguu yake minne; vikuku viwili upande mmoja, na vikuku viwili upande wake wa pili. 13 Nawe fanya miti mirefu ya mshita na kuifunika dhahabu. 14 Nawe tia hiyo miti katika vile vikuku vilivyo katika pande mbili za sanduku ili kulichukua hilo sanduku. 15 Hiyo miti itakaa katika vile vikuku vya sanduku; haitaondolewa. 16 Kisha tia ndani ya sanduku huo ushuhuda nitakaokupa. 17 Nawe fanya kiti cha rehema cha dhahabu safi; urefu wake utakuwa dhiraa mbili na nusu, na upana wake dhiraa moja na nusu. 18 Nawe fanya makerubi mawili ya dhahabu; uyafanye ya kazi ya kufua, katika hiyo miisho ya kiti cha rehema, huku na huku. 19 Weka kerubi moja mwisho mmoja, na kerubi la pili mwisho wa pili; fanya hayo makerubi ya kitu kimoja na kiti cha rehema, mwisho huku na mwisho huku. 20 Na hayo makerubi yatainua mabawa yao juu, na kukifunika hicho kiti cha rehema kwa mabawa yao, na nyuso zao zitaelekeana hili na hili; nyuso za hayo makerubi zitaelekea kiti cha rehema. 21 Weka kiti cha rehema juu ya hilo sanduku, kisha utie huo ushuhuda nitakaokupa ndani ya sanduku. 22 Nami nitaonana nawe hapo, na kuzungumza nawe pale nilipo juu ya kiti cha rehema, katikati ya hayo makerubi mawili yaliyo juu ya sanduku la ushuhuda, katika mambo yote nitakayokuagiza kwa ajili ya wana wa Israeli. 23 Nawe fanya meza ya mti wa mshita; urefu wake utakuwa dhiraa mbili, na upana wake dhiraa moja, na kwenda juu kwake dhiraa moja na nusu. 24 Uifunike dhahabu safi, na kuifanyia ukingo wa dhahabu wa kuizunguka pande zote. 25 Kisha ifanyie upapi wa kuizunguka pande zote, upana wake utakuwa nyanda nne, nawe uufanyie ule upapi ukingo wa urembo wa dhahabu wa kuuzunguka pande zote. 26 Uifanyie vikuku vinne vya dhahabu, na kuvitia vile vikuku katika pembe zake nne, katika miguu yake minne. 27 Vile vikuku na viwe karibu na ule upapi, ili viwe mahali pa kutilia ile miti, ya kuichukulia meza. 28 Fanya ile miti ya mti wa mshita, na kuifunika dhahabu, kwamba ile meza ichukuliwe kwayo. 29 Nawe fanya sahani zake, na miiko yake, na makopo yake, na vikombe vyake vya kumiminia; vifanye vyote vya dhahabu safi. 30 Nawe utaiweka mikate ya wonyesho juu ya meza mbele yangu daima. 31 Nawe fanya kinara cha taa cha dhahabu safi; hicho kinara na kifanywe cha kazi ya kufua, tako lake, na mti wake, vikombe vyake, na matovu yake, na maua yake, vyote vitakuwa vya kitu kimoja nacho; 32 nacho kitakuwa na matawi sita yenye kutoka ubavuni mwake; matawi matatu ya kinara upande wake mmoja, na matawi matatu ya kinara upande wake wa pili 33 vikombe vitatu vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi katika tawi moja; tovu na ua; na vikombe vitatu vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi katika tawi la pili, tovu na ua; vivyo hivyo hayo matawi yote sita yatokayo katika kile kinara; 34 na katika hicho kinara vikombe vinne vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi, matovu yake, na maua yake; 35 na tovu chini ya matawi mawili la kitu kimoja nacho, na tovu chini ya matawi mawili la kitu kimoja nacho, na tovu chini ya matawi mawili la kitu kimoja nacho, kwa hayo matawi sita yatokayo katika kile kinara. 36 Matovu yake na matawi yake yatakuwa ya kitu kimoja nacho; kiwe chote pia kazi moja ya kufua, ya dhahabu safi. 37 Nawe zifanye taa zake saba; nao wataziwasha hizo taa zake, zitoe nuru mbele yake. 38 Na makoleo yake, na visahani vyake, vyote vitakuwa vya dhahabu safi. 39 Kitafanywa cha talanta moja ya dhahabu safi, pamoja na vyombo hivi vyote. 40 Nawe angalia ya kwamba uvifanye kama mfano wake, ulioonyeshwa mlimani.

Kutoka 26

1 Kisha fanya hiyo maskani iwe na mapazia kumi; ifanye ya nguo ya kitani nzuri ya kusokota, pamoja na nyuzi za rangi ya samawi, na ya zambarau, na nyekundu, pamoja na makerubi; kazi ya fundi stadi. 2 Urefu wa kila pazia utakuwa dhiraa ishirini na nane, na upana wa kila pazia utakuwa dhiraa nne; mapazia yote yatakuwa ya kipimo kimoja. 3 Mapazia matano yataungwa pamoja, hili na hili; na mapazia matano mengine yataungwa pamoja, hili na hili. 4 Kisha utafanya tanzi za rangi ya samawi upande wa mwisho wa pazia moja katika ule upindo wa fungu lake, vivyo utafanya upande wa mwisho wa ile pazia iliyo, katika fungu la pili. 5 Fanya matanzi hamsini katika pazia moja, na matanzi hamsini katika upande wa mwisho wa ile pazia iliyo katika kuungana kwa pili; hizo tanzi zitaelekeana. 6 Kisha ufanye vifungo hamsini vya dhahabu, na kuunganya hayo mapazia pamoja kwa vile vifungo; na hiyo maskani itakuwa ni moja. 7 Nawe fanya mapazia ya singa za mbuzi yawe hema juu ya maskani; fanya mapazia kumi na moja. 8 Urefu wa kila pazia utakuwa dhiraa thelathini, na upana wa kila pazia utakuwa dhiraa nne; hayo mapazia kumi na moja yatakuwa ya kipimo kimoja. 9 Kisha utaunganya mapazia matano mbali, na mapazia sita mbali, na lile pazia la sita utalipeta hapo upande wa mbele wa ile hema. 10 Fanya tanzi hamsini upande wa mwisho wa pazia lile lililo la mwisho katika hayo yaliyounganywa pamoja, na tanzi hamsini upande wa mwisho wa lile pazia lililo nje katika hayo ya pili yaliyounganywa pamoja. 11 Tena ufanye vifungo hamsini vya shaba, na kuvitia vile vifungo katika zile tanzi, na kuiunganya ile hema pamoja, ili iwe hema moja. 12 Na kipande kile kilichosalia, kile kiangukacho, cha yale mapazia ya hema, ile nusu ya pazia iliyosalia, itaanguka huko upande wa nyuma wa maskani. 13 Na hiyo dhiraa moja upande mmoja, na ile dhiraa moja upande wa pili, ya urefu wa mapazia ya hema uliosalia, zitaanguka katika ubavu wa maskani upande huu na upande huu, ili kuifunika. 14 Nawe fanya kifuniko cha ile hema, cha ngozi za kondoo waume zilizotiwa rangi nyekundu, na juu yake kifuniko cha ngozi za pomboo. 15 Nawe fanya hizo mbao za maskani za mti wa mshita, zenye kusimama. 16 Kila ubao utakuwa na urefu wa dhiraa kumi, na upana wake kila ubao utakuwa dhiraa moja na nusu. 17 Kila ubao utakuwa na ndimi mbili, zenye kuunganywa huu na huu; ndivyo utakavyozifanya mbao zote za maskani. 18 Kisha ufanye zile mbao za maskani, mbao ishirini kwa upande wa kusini kuelekea kusini. 19 Nawe ufanye matako arobaini ya fedha chini ya zile mbao ishirini, matako mawili chini ya ubao mmoja, kupokea zile ndimi zake mbili, na matako mawili chini ya ubao mwingine kupokea zile ndimi zake mbili; 20 na upande wa pili wa maskani, upande wa kaskazini, mbao ishirini; 21 na matako yake ya fedha arobaini; matako mawili chini ya ubao mmoja, na matako mawili chini ya ubao mwingine. 22 Kisha ufanye mbao sita kwa ajili ya upande wa nyuma wa maskani kuelekea magharibi. 23 Tena ufanye mbao mbili kwa ajili ya hizo pembe za maskani zilizo upande wa nyuma. 24 Upande wa chini zitakuwa ni mbili mbili; vivyo zitaungwa pamoja mbao pacha hata ncha ya juu katika pete ya kwanza; zote mbili ndivyo zitakavyokuwa; zitakuwa kwa ajili ya hizo pembe mbili. 25 Mbao zitakuwa ni nane, na matako yake ya fedha, matako kumi na sita; matako mawili chini ya ubao mmoja, na matako mawili chini ya ubao wa pili. 26 Nawe fanya mataruma ya mti wa mshita; mataruma matano kwa ajili ya mbao za upande mmoja wa maskani, 27 na mataruma matano kwa ajili ya mbao za upande wa pili wa maskani, na mataruma matano kwa ajili ya mbao za upande wa maskani ulio nyuma kuelekea magharibi. 28 Na hilo taruma la katikati, lililo katikati ya zile mbao litapenya toka mwisho huu hata mwisho huu. 29 Na hizo mbao utazifunika dhahabu, na pete zake za kutilia yale mataruma utazifanya za dhahabu; na hayo mataruma utayafunika dhahabu. 30 Nawe utaisimamisha hiyo maskani sawasawa na mfano wake ulioonyeshwa mlimani. 31 Nawe fanya pazia la nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na nguo za kitani nzuri zenye kusokotwa, litafumwa na kutiwa makerubi, kazi ya fundi stadi; 32 kisha litungike katika nguzo nne za mti wa mshita zilizofunikwa dhahabu, vifungo vyake vitakuwa vya dhahabu, katika matako ya fedha manne. 33 Nawe tungika lile pazia chini ya vile vifungo, nawe lete lile sanduku la ushuhuda na kulitia humo nyuma ya pazia; na lile pazia litawagawanyia kati ya patakatifu, na mahali patakatifu sana. 34 Nawe utaweka kiti cha rehema juu ya lile sanduku la ushuhuda ndani ya mahali pale patakatifu sana. 35 Na ile meza utaiweka nje ya pazia, na kinara cha taa kuikabili ile meza upande wa maskani wa kuelekea kusini; na ile meza utaiweka upande wa kaskazini. 36 Kisha utafanya kisitiri kwa mlango wa Hema, cha nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na kitani nzuri yenye kusokotwa, kazi ya mshona taraza. 37 Nawe fanya nguzo tano za mti wa mshita kwa kile kisitiri, na kuzifunika dhahabu; kulabu zake zitakuwa za dhahabu; nawe utasubu matako ya shaba matano kwa ajili yake.

Kutoka 27

1 Nawe fanya madhabahu ya mti wa mshita; urefu wake utakuwa ni dhiraa tano, na upana wake dhiraa tano; hiyo madhabahu itakuwa mraba; na kwenda juu kwake kutakuwa dhiraa tatu. 2 Nawe fanya pembe nne katika pembe zake nne; hizo pembe zitakuwa za kitu kimoja na madhabahu; nawe utayafunika shaba. 3 Na vyombo vyake vya kuyaondoa majivu yake utavifanya, na majembe yake, na mabakuli yake, na uma zake, na meko yake; vyombo vyake vyote utavifanya vya shaba. 4 Nawe uifanyie hiyo madhabahu wavu wa shaba; kisha utie pete nne za shaba katika hizo pembe nne za ule wavu. 5 Nawe tia huo wavu chini ya kizingo kiizungukacho madhabahu upande wa chini, ili huo wavu ufikilie katikati ya hiyo madhabahu. 6 Nawe fanya miti kwa ajili ya madhabahu, miti ya mshita, na kuifunika shaba. 7 Na hiyo miti itatiwa katika pete, na ile miti itakuwa katika pande mbili za madhabahu, wakati wa kuichukua. 8 Uifanye ya mbao, yenye mvungu ndani yake; kama ulivyoonyeshwa mlimani, ndivyo watakavyoifanya. 9 Nawe fanya ua wa maskani; upande wa kusini wa kuelekea kusini kutakuwa na chandarua ya nguo ya kitani nzuri yenye kusokotwa, kwa huo ua, urefu wake upande mmoja utakuwa ni dhiraa mia; 10 na nguzo zake zitakuwa nguzo ishirini, na matako yake ishirini, matako yake yatakuwa ya shaba; kulabu za zile nguzo na vitanzi vyake vitakuwa vya fedha. 11 Ni vivyo upande wa kaskazini, urefu wake hiyo chandarua utakuwa ni dhiraa mia, na nguzo zake ishirini, na matako yake ishirini yatakuwa ya shaba; kulabu za zile nguzo na vitanzi vyake vitakuwa vya fedha. 12 Na upande wa magharibi, upana wa ua kutakuwa na chandarua ya dhiraa hamsini; nguzo zake kumi, na matako yake kumi. 13 Na upana wa ule ua upande wa mashariki kuelekea mashariki utakuwa ni dhiraa hamsini. 14 Chandarua upande mmoja wa lango itakuwa dhiraa kumi na tano upana wake; nguzo zake zitakuwa tatu na matako yake matatu. 15 Upande wa pili ni vivyo chandarua ya dhiraa kumi na tano; nguzo zake tatu, na matako yake matatu. 16 Na kwa lile lango la ua patakuwa na kisitiri cha dhiraa ishirini, kitakuwa cha nguo ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri yenye kusokotwa, kazi ya mshona taraza; nguzo zake zitakuwa nne, na matako yake manne. 17 Nguzo zote za ule ua ziuzungukazo pande zote zitakuwa na vitanzi vya fedha; kulabu zake za fedha, na matako yake ya shaba. 18 Urefu wa huo ua utakuwa dhiraa mia, na upana wake utakuwa dhiraa hamsini kotekote, na kwenda juu kwake dhiraa tano; yawe ya nguo ya kitani nzuri, na matako yake yatakuwa ya shaba. 19 Vyombo vyote vya maskani vitumiwavyo katika utumishi wake wote, na vigingi vyake vyote, na vigingi vyote vya ule ua, vitakuwa vya shaba. 20 Nawe waamuru wana wa Israeli wakuletee mafuta ya zeituni safi ya kupondwa kwa ajili ya nuru, ili kufanya ile taa kuwaka daima. 21 Ndani ya ile hema ya kukutania, nje ya hilo pazia, lililo mbele ya huo ushuhuda, Haruni na wanawe wataitengeza tangu jioni hata asubuhi mbele ya Bwana; itakuwa ni amri ya milele katika vizazi vyao vyote kwa ajili ya wana wa Israeli.

Kutoka 28

1 Nawe umlete Haruni ndugu yako karibu nami, na wanawe pamoja naye, miongoni mwa wana wa Israeli, ili anitumikie katika kazi ya ukuhani. Haruni, na Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari, wana wa Haruni. 2 Nawe utamfanyia Haruni ndugu yako mavazi matakatifu, kwa utukufu na kwa uzuri. 3 Nawe utawaambia watu wote wenye moyo wa hekima, niliowajaza na roho ya hekima wamfanyie Haruni mavazi ili kumtakasa anitumikie katika kazi ya ukuhani. 4 Na mavazi watakayoyafanya ni haya; kifuko cha kifuani, na naivera, na joho, na kanzu ya kazi ya urembo; na kilemba, na mshipi; nao watawafanyia Haruni nduguyo, na wanawe, mavazi matakatifu ili anitumikie katika kazi ya ukuhani. 5 Nao wataitwaa dhahabu, na nguo ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na ya rangi nyekundu, na nguo ya kitani nzuri. 6 Nao waifanye naivera kwa nyuzi za dhahabu, na za samawi, na za zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri yenye kusokotwa kwa kazi ya mstadi. 7 Itakuwa na vipande viwili vya mabegani, vilivyoungana kwenye ncha zake mbili; ili ipate kuunganywa. 8 Na mshipi wa kazi ya ustadi ulio juu yake, ili kuifunga mahali pake; utakuwa wa kazi kama ile ya naivera, ya vitu vile vile ya nyuzi za dhahabu, na za rangi ya samawi, na ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri yenye kusokotwa. 9 Nawe utatwaa vito viwili vya shohamu, ya rangi ya chani-kiwiti, nawe utachora juu yake majina ya wana wa Israeli; 10 majina yao sita katika kito kimoja, na majina sita yaliyosalia katika kile kito cha pili, kwa utaratibu wa kuzaliwa kwao. 11 Kwa kazi mtu mwenye kuchora mawe kama vile muhuri ichorwavyo, utavichora hivi vito viwili, sawasawa na majina ya wana wa Israeli, nawe utavitia katika vijalizo vya dhahabu. 12 Nawe utavitia vile vito viwili juu ya vipande vya mabegani vya hiyo naivera, viwe vito vya ukumbusho kwa ajili ya wana wa Israeli; naye Haruni atayachukua majina yao mbele za Bwana juu ya mabega yake mawili ili kuwa ukumbusho. 13 Nawe fanya vijalizo viwili vya dhahabu; 14 na mikufu miwili ya dhahabu safi; utaifanya iwe mfano wa kamba, ya kazi ya kusokotwa; nawe uitie ile mikufu ya kazi ya kusokotwa katika vile vijalizo. 15 Nawe utafanya kifuko cha kifuani cha hukumu, kazi ya fundi stadi; utakifanya kwa kuiandama ile kazi ya hiyo naivera; ya nyuzi za dhahabu, na za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani safi yenye kusokotwa, ndivyo utakavyokifanya. 16 Kitakuwa mraba, tena cha kukunjwa; urefu wake utakuwa shibiri moja, na upana wake shibiri moja. 17 Nawe ukijaze viweko vya vito, safu nne za vito; safu moja itakuwa ni akiki, na yakuti ya rangi ya manjano, na baharamani, hivi vitakuwa safu ya kwanza; 18 na safu ya pili itakuwa zumaridi, na yakuti samawi, na almasi; 19 na safu ya tatu itakuwa hiakintho, na akiki nyekundu, na amethisto; 20 na safu ya nne itakuwa ni zabarajadi, na shohamu, na yaspi; vito hivyo vitakazwa ndani ya dhahabu kwa kujaa mahali pake. 21 Na vile vito vitakuwa sawasawa na majina ya wana wa Israeli, kumi na viwili, sawasawa na majina yao; mfano wa kuchora kwa muhuri kila kimoja sawasawa na jina lake, vitakuwa vya hizo kabila kumi na mbili. 22 Nawe utie katika kile kifuko cha kifuani mikufu mfano wa kamba, ya kazi ya kusokotwa, ya dhahabu safi. 23 Nawe utie pete mbili za dhahabu katika kile kifuko cha kifuani, na kuzitia hizo pete mbili katika ncha mbili za kifuko cha kifuani. 24 Nawe utie hiyo mikufu miwili ya dhahabu iliyosokotwa katika zile pete mbili zilizo katika ncha za kifuko cha kifuani. 25 Na ncha zile nyingine za hiyo mikufu miwili ya kusokotwa utazitia katika vile vijalizo viwili, na kuvitia katika vile vipande vya mabegani vya naivera upande wa mbele. 26 Nawe utafanya pete mbili za dhahabu, uzitie katika hizo ncha mbili za kifuko cha kifuani, katika ukingo wake, ulio upande wa naivera ulio ndani. 27 Nawe fanya pete mbili za dhahabu, na kuzitia katika vile vipande viwili vya mabegani vya ile naivera chini yake, upande wa mbele, karibu na kifungo chake, juu ya huo mshipi wa naivera uliosukwa kwa ustadi. 28 Nao watakikaza kile kileso kwa zile pete zake kwenye pete za naivera kwa ukanda wa rangi ya samawi, ili kwamba kikae pale juu ya ule mshipi wa naivera uliosukwa kwa ustadi, ili kwamba kifuko cha kifuani kisiachane na naivera. 29 Na Haruni atayachukua majina ya wana wa Israeli katika kile kifuko cha kifuani cha hukumu juu ya moyo wake, hapo atakapoingia ndani ya mahali patakatifu, kuwa ukumbusho mbele ya Bwana daima. 30 Nawe utie hizo Urimu na Thumimu katika kile kifuko cha kifuani cha hukumu; nazo zitakuwa juu ya moyo wa Haruni, hapo atakapoingia ndani mbele ya Bwana; na Haruni atachukua hukumu ya hao wana wa Israeli juu ya moyo wake mbele ya Bwana daima. 31 Nawe fanya hiyo joho ya naivera ya rangi ya samawi yote. 32 Nayo itakuwa na tundu katikati yake kwa kupitisha kichwa; itakuwa na utepe wa kazi ya kusokotwa kuzunguka hilo tundu lake, mfano wa tundu lililo katika kanzu ya chuma, ili lisipasuke. 33 Nawe katika pindo zake utatia makomamanga ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na ya rangi nyekundu, kuzunguka pindo zake kotekote; na njuga za dhahabu kati ya hayo makomamanga pande zote; 34 njuga ya dhahabu na komamanga, njuga ya dhahabu na komamanga, katika pindo za joho kuizunguka pande zote. 35 Nayo itakuwa juu ya Haruni akitumika; na sauti ya hizo njuga itasikilikana hapo aingiapo ndani ya mahali patakatifu mbele ya Bwana na hapo atokapo nje, ili kwamba asife. 36 Nawe fanya bamba la dhahabu safi na kuchora juu yake, mfano wa machoro ya muhuri, MTAKATIFU KWA Bwana. 37 Nawe ulitie hilo bamba katika ukanda wa rangi ya samawi, nalo litakuwa katika kile kilemba; litakuwa upande wa mbele wa kile kilemba. 38 Nalo litakuwa katika kipaji cha uso cha Haruni, na Haruni atauchukua uovu wa vile vitu vitakatifu, watakavyovitakasa hao wana wa Israeli katika vipawa vyao vyote vitakatifu, nalo litakuwa katika kipaji chake cha uso sikuzote, ili kwamba vipate kukubaliwa mbele za Bwana. 39 Na hiyo kanzu utaifuma ya kitani nzuri ya kazi ya urembo, ufanye na kilemba cha nguo ya kitani nzuri, nawe utafanya mshipi wa kazi ya mwenye kutia taraza. 40 Kisha utafanya kanzu kwa ajili ya wana wa Haruni, nawe wafanyie mishipi, wafanyie na kofia kwa utukufu na uzuri. 41 Nawe mvike huyo nduguyo Haruni na wanawe nao mavazi hayo; nawe watie mafuta, na kuwaweka kwa kazi takatifu, na kuwatakasa, ili wapate kunitumikia mimi katika kazi ya ukuhani. 42 Nawe wafanyie suruali za nguo ya kitani, ili kufunika tupu ya miili yao; suruali hizo zitafika tangu kiunoni hata mapajani; 43 na Haruni na wanawe watazivaa, hapo watakapoingia katika hema ya kukutania, au hapo watakapoikaribia madhabahu ili watumike katika mahali patakatifu; wasije wakachukua uovu, wakafa; hii itakuwa ni amri ya milele kwake yeye, na kwa wazao wake.

Kutoka 29

1 Nawe uwafanyie jambo hili, ili kuwatakasa, wapate kunitumikia mimi katika kazi ya ukuhani; twaa ng'ombe mmoja mume kijana, na kondoo waume wawili walio wakamilifu, 2 na mkate usiotiwa chachu, na maandazi yasiyotiwa chachu yaliyokandwa kwa mafuta, na kaki zisizotiwa chachu zilizotiwa mafuta; utazifanya za unga mzuri mwembamba wa ngano. 3 Nawe vitie vyote katika kikapu, uvilete ndani ya kikapu, pamoja na huyo ng'ombe, na hao kondoo waume wawili. 4 Kisha mlete Haruni na wanawe hata mlangoni pa hema ya kukutania, ukawaoshe kwa maji. 5 Kisha twaa hayo mavazi na kumvika Haruni; itie kanzu, na joho ya naivera, na naivera, na kifuko cha kifuani, na kumkaza kwa huo mshipi wa naivera uliosukwa kwa ustadi; 6 nawe mvike kile kilemba kichwani, na ile taji takatifu utaitia katika kile kilemba. 7 Ndipo utakapotwaa hayo mafuta ya kutiwa, na kummiminia kichwani mwake, na kumtia mafuta. 8 Kisha walete hao wanawe na kuwavika kanzu. 9 Nawe uwakaze mishipi, Haruni na wanawe, na kuwavika kofia; nao watakuwa na huo ukuhani kwa amri ya milele; nawe utawaweka Haruni na wanawe kwa kazi takatifu. 10 Kisha utamleta huyo ng'ombe mbele ya hema ya kukutania; na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo ng'ombe. 11 Kisha utamchinja huyo ng'ombe mbele ya Bwana, mlangoni pa hema ya kukutania. 12 Kisha twaa baadhi ya damu ya ng'ombe, uitie katika pembe za madhabahu kwa kidole chako; na kuimimina damu yote chini ya madhabahu. 13 Kisha twaa mafuta yote yafunikayo matumbo, na kitambi kilicho katika ini, na figo mbili, na mafuta yaliyo juu yake, uyateketeze yote juu ya madhabahu. 14 Lakini nyama yake huyo ng'ombe, na ngozi yake, na mavi yake, utayachoma kwa moto nje ya marago; ni sadaka kwa ajili ya dhambi. 15 Pia mtwae kondoo mume mmoja; na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa chake huyo kondoo mume. 16 Kisha utamchinja huyo kondoo mume, na kuitwaa damu yake, na kuinyunyiza katika madhabahu kuizunguka kando-kando. 17 Kisha utamkata-kata kondoo vipande vyake, na kuyaosha matumbo yake na miguu yake, na kuiweka pamoja na vipande vyake na kichwa chake. 18 Nawe mteketeze kondoo mzima juu ya madhabahu; ni sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya Bwana; ni harufu nzuri, sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 19 Kisha mtwae huyo kondoo wa pili; na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa chake huyo kondoo. 20 Kisha utamchinja kondoo, na kuitwaa damu yake, na kuitia katika ncha ya sikio la Haruni la upande wa kuume, na katika ncha za masikio ya kuume ya wanawe, na katika vyanda vya gumba vya mikono yao ya kuume, na katika vidole vikuu vya miguu yao ya kuume, na kuinyunyiza hiyo damu katika madhabahu kuizunguka kando-kando. 21 Kisha twaa katika hiyo damu iliyo juu ya madhabahu, na katika hayo mafuta ya kutiwa, na kumnyunyizia Haruni, juu ya mavazi yake, na wanawe, na mavazi yao pia, pamoja naye; naye atatakaswa, na mavazi yake, na wanawe, na mavazi ya wanawe, pamoja naye. 22 Tena yatwae mafuta ya huyo kondoo mume, na mkia wake wa mafuta, na mafuta yafunikayo matumbo, na kitambi kilicho katika ini, na figo mbili, na mafuta yaliyo katika hizo figo, na paja la kuume; kwani ni kondoo ambaye ni wa kuwekwa kwa kazi takatifu; 23 utwae na mkate mmoja wa unga, na mkate mmoja ulioandaliwa kwa mafuta, na kaki moja katika kile kikapu cha mikate isiyotiwa chachu, kilichowekwa mbele ya Bwana; 24 nawe utavitia hivi vyote katika mikono ya Haruni, na katika mikono ya wanawe; nawe utavitikisa-tikisa viwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana. 25 Kisha uvitwae vile vitu mikononi mwao, na kuviteketeza juu ya madhabahu, juu ya ile sadaka ya kuteketezwa, viwe harufu nzuri mbele ya Bwana; ni sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 26 Kisha twaa kidari cha huyo kondoo wa kuwekwa kwake Haruni kwa kazi takatifu, na kukitikisa-tikisa kiwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana; nacho kitakuwa ni sehemu yako. 27 Nawe kitakase kile kidari cha ile sadaka ya kutikiswa, na lile paja la sadaka ya kuinuliwa, lililotikiswa, na lililoinuliwa juu, vya yule kondoo wa kuwekwa kwa kazi takatifu, huyo aliyekuwa kwa ajili ya Haruni, na huyo aliyekuwa kwa ajili ya wanawe; 28 navyo vitakuwa vya Haruni na wanawe posho ya lazima sikuzote itokayo kwa hao wana wa Israeli; kwa kuwa ni sadaka ya kuinuliwa; nayo itakuwa ni sadaka ya kuinuliwa itokayo kwa hao wana wa Israeli katika dhabihu zao za sadaka za amani, ni sadaka yao ya kuinuliwa kwa ajili ya Bwana. 29 Na hayo mavazi matakatifu ya Haruni yatakuwa ya wanawe baada yake, wayavae watakapotiwa mafuta, na watakapowekwa kwa kazi takatifu. 30 Huyo mwanawe atakayekuwa kuhani badala yake atayavaa muda wa siku saba, hapo atakapoingia ndani ya hiyo hema ya kukutania, ili atumike ndani ya mahali patakatifu. 31 Nawe twaa huyo kondoo mume aliyekuwa wa kuwekwa kwa kazi takatifu, na kuitokosa nyama yake katika mahali patakatifu. 32 Na Haruni na wanawe wataila ile nyama ya kondoo, na mikate iliyo katika kile kikapu, hapo mbele ya mlango wa hema ya kukutania. 33 Nao watakula vile vitu ambavyo upatanisho ulifanywa kwa hivyo, ili kuwaweka kwa kazi takatifu na kuwatakasa; lakini mgeni asivile, maana, ni vitu vitakatifu. 34 Na kwamba kitu cho chote cha ile nyama, iliyo kwa ajili ya kuweka kwa kazi takatifu, au cho chote cha hiyo mikate, kikisalia hata asubuhi, ndipo utavichoma kwa moto hivyo vilivyosalia; havitaliwa, maana, ni vitu vitakatifu. 35 Ni hivyo utakavyowatendea Haruni na wanawe, sawasawa na hayo yote niliyokuagiza; utawaweka kwa kazi takatifu siku saba. 36 Kila siku utamtoa ng'ombe wa sadaka ya dhambi kwa ajili ya upatanisho; nawe utaisafisha hiyo madhabahu, hapo utakapofanya upatanisho kwa ajili ya hiyo madhabahu; nawe utaitia mafuta, ili kuitakasa. 37 Utafanya upatanisho kwa ajili ya hiyo madhabahu muda wa siku saba, na kuitakasa; ndipo madhabahu itakapokuwa takatifu sana; kila kitu kiigusacho madhabahu kitakuwa kitakatifu. 38 Basi sadaka utakazozitoa juu ya madhabahu ni hizi; wana-kondoo wa mwaka mmoja wawili siku baada ya siku daima. 39 Mwana-kondoo mmoja utamchinja asubuhi; na mwana-kondoo wa pili utamchinja jioni; 40 tena, pamoja na mwana-kondoo mmoja utatoa vibaba vitatu vya unga mzuri uliochanganyika na mafuta yenye kupondwa, kiasi cha kibaba na robo kibaba; na divai kiasi cha kibaba na robo kibaba, iwe sadaka ya kinywaji. 41 Na huyo mwana-kondoo wa pili utamchinja wakati wa jioni, nawe utamfanyia vivyo kama ile sadaka ya unga ya asubuhi, na kama ile sadaka yake ya kinywaji, iwe harufu nzuri, ni dhabihu ya kusongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 42 Itakuwa ni sadaka ya kuteketezwa milele katika vizazi vyenu vyote mlangoni pa ile hema ya kukutania mbele ya Bwana; hapo nitakapokutana nanyi, ili ninene na wewe hapo. 43 Nami nitakutana na wana wa Israeli hapo, na hiyo Hema itafanywa takatifu na utukufu wangu. 44 Nami nitaitakasa hiyo hema ya kukutania, na hiyo madhabahu; pia Haruni na wanawe nitawatakasa, ili wanitumikie katika kazi ya ukuhani. 45 Na mimi nitakaa kati ya wana wa Israeli, nami nitakuwa Mungu wao. 46 Nao watanijua kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wao, niliyewaleta watoke katika nchi ya Misri, nipate kukaa kati yao; ni mimi Bwana Mungu wao.

Kutoka 30

1 Nawe fanya madhabahu ya kufukizia uvumba; utaifanyiza kwa mti wa mshita. 2 Urefu wake utakuwa dhiraa moja, na upana wake dhiraa moja; itakuwa mraba; na kwenda juu kwake dhiraa mbili; pembe zake zitakuwa za kitu kimoja nayo. 3 Nawe utaifunikiza dhahabu safi juu yake, na mbavu zake kando kando, na pembe zake; nawe utaifanyia ukingo wa dhahabu kuizunguka. 4 Kisha utaifanyia pete mbili za dhahabu, chini ya ukingo wake katika mbavu zake mbili, katika pande zake mbili utazifanya; nazo zitakuwa mahali pa kuitia miti ya kuichukulia. 5 Na ile miti utaifanya kwa mti wa mshita, na kuifunikiza dhahabu safi. 6 Nawe utaitia mbele ya lile pazia lililo karibu na sanduku la ushuhuda mbele ya kiti cha rehema kilicho juu ya ushuhuda, hapo nitakapokutana nawe. 7 Na Haruni atafukiza uvumba wa manukato juu yake; kila siku asubuhi atakapozitengeneza zile taa, ataufukiza. 8 Na Haruni atakapoziwasha zile taa wakati wa jioni, ataufukiza, uwe uvumba wa daima mbele za Bwana katika vizazi vyenu vyote. 9 Hamtafukiza juu yake uvumba mgeni, wala sadaka ya kuteketezwa, wala sadaka ya unga, wala hamtamimina juu yake sadaka ya kinywaji. 10 Naye Haruni atafanya upatanisho juu ya pembe zake mara moja kila mwaka; kwa damu ya ile sadaka ya dhambi ya kufanya upatanisho, mara moja kila mwaka ataifanyia upatanisho, katika vizazi vyenu vyote; ni takatifu sana kwa Bwana. 11 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 12 Utakapowahesabu wana wa Israeli, kama itakavyotokea hesabu yao, ndipo watakapompa Bwana kila mtu ukombozi kwa ajili ya roho yake, hapo utakapowahesabu; ili kwamba yasiwe maradhi kati yao, hapo utakapowahesabu. 13 Nacho watakachotoa ni hiki, kila mtu apitaye kwa wale waliohesabiwa atatoa nusu shekeli kwa kuiandama shekeli ya mahali patakatifu; (shekeli ni gera ishirini;) nusu shekeli kwa sadaka ya Bwana. 14 Kila mtu apitaye kwa wale waliohesabiwa tangu huyo ambaye umri wake ni miaka ishirini, au zaidi, atatoa hiyo sadaka ya Bwana. 15 Matajiri hawataleta zaidi, wala maskini hawataleta kilichopungua, katika hiyo nusu shekeli, watakapotoa hiyo sadaka ya Bwana, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya roho zenu. 16 Nawe utapokea hizo fedha za upatanisho mikononi mwa hao wana wa Israeli, na kuziweka kwa ajili ya utumishi wa hema ya kukutania; ili kwamba ziwe ukumbusho kwa ajili ya wana wa Israeli mbele ya Bwana, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya roho zenu. 17 Bwana akanena na Musa, na kumwambia 18 Fanya na birika la shaba, na tako lake la shaba, ili kuogea; nawe utaliweka kati ya hema ya kukutania na madhabahu, nawe utalitia maji. 19 Na Haruni na wanawe wataosha mikono yao na miguu yao humo; 20 hapo waingiapo ndani ya hema ya kukutania; watajiosha majini, ili wasife; au hapo watakapoikaribia madhabahu ili watumike, kumteketezea Bwana sadaka ya moto; 21 basi wataosha mikono yao na miguu yao ili kwamba wasife; na neno hili litakuwa amri kwao milele, kwake yeye na kwa wazao wake katika vizazi vyao vyote. 22 Kisha Bwana akasema na Musa, na kumwambia, 23 Jitwalie manukato yaliyo bora, manemane mbichi shekeli mia tano, na mdalasini wenye harufu nzuri nusu ya kiasi hicho, yaani, shekeli mia mbili na hamsini, na kane shekeli mia mbili na hamsini, 24 na kida shekeli mia tano, kwa kuiandama shekeli ya mahali patakatifu, na mafuta ya zeituni kiasi cha vibaba vitano; 25 nawe utayafanya mafuta ya kutiwa matakatifu, marhamu iliyochanganywa kwa kazi ya ustadi ya mtengezaji manukato; yatakuwa ni mafuta matakatifu ya kutiwa. 26 Nawe utaipaka hema ya kukutania kwa mafuta hayo, na hilo sanduku la ushuhuda, 27 na hiyo meza, na vyombo vyake vyote, na kinara cha taa, na vyombo vyake, na madhabahu ya kufukizia uvumba, 28 na madhabahu ya kuteketezea sadaka, pamoja na vyombo vyake vyote, na birika, na tako lake. 29 Nawe utavitakasa vitu hivyo, ili viwe vitakatifu sana; tena kila kivigusacho vyombo vile kitakuwa kitakatifu. 30 Nawe utawatia mafuta Haruni na wanawe, na kuwatakasa, ili wanitumikie katika kazi ya ukuhani. 31 Nawe utanena na wana wa Israeli na kuwaambia, Haya yatakuwa ni mafuta matakatifu ya kutiwa kwa ajili yangu mimi katika vizazi vyenu vyote. 32 Hayatamiminwa katika kiwiliwili cha binadamu, wala msifanye mengine mfano wa haya kama yalivyoungwa kwa viungo vyake; ni matakatifu, na kwenu ninyi yatakuwa matakatifu. 33 Mtu awaye yote atakayechanganya mafuta mfano wa haya, au mtu awaye yote atakayetia mafuta haya juu ya mgeni, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake. 34 Bwana akamwambia Musa, Jitwalie manukato mazuri, yaani, natafi, na shekelethi, na kelbena; viungo vya manukato vizuri pamoja na ubani safi; vitu hivyo vyote na viwe vya kipimo kimoja; 35 nawe utafanya uvumba wa vitu hivyo, manukato ya kazi ya ustadi wa mtengenazaji manukato, yatakuwa yamekolea, safi, matakatifu; 36 nawe baadhi yake utayaponda sana, na kuyaweka mbele ya ushuhuda ndani ya hema ya kukutania, hapo nitakapokutana nawe; nayo yatakuwa kwenu matakatifu sana. 37 Na uvumba utakaofanya, hamtajifanyia uvumba wenye viungo sawasawa na uvumba huo; utakuwa kwenu mtakatifu kwa ajili ya Bwana. 38 Mtu ye yote atakayefanya mfano wa huo, ili kuunusa, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake.

Kutoka 31

1 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Angalia, nimemwita kwa jina lake Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda; 3 nami nimemjaza roho ya Mungu, katika hekima, na maarifa, na ujuzi, na mambo ya kazi ya kila aina, 4 ili abuni kazi za ustadi, kuwa fundi wa dhahabu, na wa fedha, na wa shaba, 5 na kukata vito kwa kutiwa mahali, na kuchora miti, na kufanya kazi ya ustadi iwayo yote. 6 Tena, tazama, nimemchagua, awe pamoja naye, huyo Oholiabu, mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani; nami nimetia hekima katika mioyo ya wote wenye moyo wa hekima, ili wapate kufanya vyote nilivyokuagiza; 7 yaani, hema ya kukutania na sanduku la ushuhuda, na kiti cha rehema kilicho juu yake, na vyombo vyote vya Hema; 8 na meza, na vyombo vyake, na kinara cha taa safi pamoja na vyombo vyake vyote, na madhabahu ya kufukizia uvumba; 9 na madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na vyombo vyake vyote, na birika na tako lake; 10 na mavazi yenye kufumwa kwa uzuri, na mavazi matakatifu ya Haruni kuhani, na mavazi ya wanawe, ili kutumika katika kazi ya ukuhani; 11 na mafuta ya kutiwa, na uvumba wa manukato mazuri, kwa ajili ya mahali patakatifu; sawasawa na yote niliyokuagiza ndivyo watakavyofanya wao. 12 Bwana akasema na Musa, na kumwambia, 13 Kisha, nena wewe na wana wa Israeli, na kuwaambia, Hakika mtazishika Sabato zangu, kwa kuwa ni ishara kati ya mimi na ninyi katika vizazi vyenu vyote; ili mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana niwatakasaye ninyi. 14 Basi mtaishika hiyo Sabato; kwa kuwa ni takatifu kwenu; kila mtu atakayeitia unajisi hakika yake atauawa; kwa kuwa kila mtu afanyaye kazi katika siku hiyo, nafsi hiyo itakatiliwa mbali na watu wake. 15 Kazi itafanywa siku sita; lakini siku ya saba ni Sabato ya kustarehe kabisa, takatifu kwa Bwana; kila mtu atakayefanya kazi yo yote katika siku ya Sabato, hakika yake atauawa. 16 Kwa ajili ya hayo wana wa Israeli wataishika Sabato, kuiangalia sana hiyo Sabato katika vizazi vyao vyote, ni agano la milele. 17 Ni ishara kati ya mimi na wana wa Israeli milele; kwani kwa siku sita Bwana alifanya mbingu na nchi, akastarehe kwa siku ya saba na kupumzika. 18 Hapo Bwana alipokuwa amekwisha zungumza na Musa katika mlima wa Sinai, akampa hizo mbao mbili za ushuhuda, mbao mbili za mawe, zilizoandikwa kwa chanda cha Mungu.

Kutoka 32

1 Hata watu walipoona ya kuwa Musa amekawia kushuka katika mlima, wakakusanyana wakamwendea Haruni, wakamwambia, Haya! Katufanyizie miungu itakayokwenda mbele yetu, kwa maana Musa huyo aliyetutoa katika nchi ya Misri hatujui yaliyompata. 2 Haruni akawaambia, Zivunjeni pete za dhahabu zilizo katika masikio ya wake zenu, na wana wenu, na binti zenu, mkaniletee. 3 Watu wote wakazivunja pete za dhahabu zilizo katika masikio yao, wakamletea Haruni. 4 Akaipokea mikononi mwao akaitengeneza kwa patasi, akaifanya iwe sanamu ya ndama kwa kuiyeyusha; nao wakasema, Hiyo ndiyo miungu yako, Ee Israeli, iliyokutoa katika nchi ya Misri. 5 Naye Haruni alipoona jambo hili, akajenga madhabahu mbele yake; Haruni akatangaza akasema, Kesho itakuwa sikukuu kwa Bwana. 6 Wakaondoka asubuhi na mapema, wakatoa dhabihu, wakaleta sadaka za amani, watu wakaketi kula na kunywa, wakaondoka wacheze. 7 Bwana akamwambia Musa, Haya! Shuka; kwa maana watu wako uliowatoa katika nchi ya Misri wamejiharibu nafsi zao, 8 wamepotoka upesi kuiacha ile njia niliyowaamuru, wamejifanyizia ndama ya kuyeyusha wakaiabudu na kuitolea dhabihu, wakasema, Hiyo ndiyo miungu yako, Ee Israeli, iliyokutoa katika nchi ya Misri. 9 Tena Bwana akamwambia Musa, Mimi nimewaona watu hawa, na tazama, ni watu wenye shingo ngumu 10 basi sasa niache, ili hasira zangu ziwake juu yao, niwaangamize, nami nitakufanya wewe uwe taifa kuu. 11 Musa akamsihi sana Bwana, Mungu wake, na kusema, Bwana, kwa nini hasira zako kuwaka juu ya watu wako uliowaleta kutoka nchi ya Misri kwa uweza mkuu, na kwa mkono wenye nguvu? 12 Kwa nini Wamisri kunena, wakisema, Amewatoa kwa kuwatenda uovu, ili apate kuwaua milimani, na kuwaondoa watoke juu ya uso wa nchi? Geuka katika hasira yako kali, ughairi uovu huu ulio nao juu ya watu wako. 13 Mkumbuke Ibrahimu, na Isaka, na Israeli, watumishi wako, ambao uliwaapia kwa nafsi yako, na kuwaambia, Nitazidisha kizazi chenu mfano wa nyota za mbinguni; tena nchi hii yote niliyoinena nitakipa kizazi chenu nao watairithi milele. 14 Na Bwana akaughairi ule uovu aliosema ya kwamba atawatenda watu wake. 15 Basi, Musa akageuka akashuka katika mlima, na zile mbao mbili za mawe mikononi mwake; mbao zilizoandikwa pande zote mbili, upande huu na upande huu ziliandikwa. 16 Na zile mbao zilikuwa kazi ya Mungu nayo maandiko yalikuwa maandiko ya Mungu, yaliyochorwa katika zile mbao. 17 Na Yoshua aliposikia kelele za watu walipokuwa wakipiga kelele, akamwambia Musa, Kuna kelele ya vita maragoni. 18 Akasema, Hiyo si sauti ya watu wapigao kelele kwa sababu ya kushinda vitani, wala si sauti ya watu wapigao kelele kwa sababu ya kushindwa; bali kelele za watu waimbao ndizo ninazozisikia mimi. 19 Hata alipoyakaribia marago akaiona ile ndama, na ile michezo. Hasira ya Musa ikawaka, akazitupa zile mbao mikononi mwake, akazivunja chini ya mlima. 20 Akaitwaa ile ndama waliyoifanya, akaichoma moto, akaisaga hata ikawa mavumbi, akainyunyiza juu ya maji, akawanywesha wana wa Israeli. 21 Musa akamwambia Haruni Watu hawa wamekufanyani hata ukaleta dhambi hii kuu juu yao? 22 Haruni akasema, Hasira ya bwana wangu isiwake, wewe unawajua watu hawa, ya kuwa wamejielekeza kwa mabaya. 23 Maana waliniambia, Katufanyie miungu, itakayokwenda mbele yetu, kwa maana mtu huyo Musa, aliyetutoa katika nchi ya Misri, hatujui yaliyompata. 24 Nikawaambia, Mtu ye yote aliye na dhahabu na aivunje; basi wakanipa, nami nikaitupa ndani ya moto, akatoka ndama huyu. 25 Basi Musa alipoona ya kuwa watu hawa wameasi, maana Haruni amewaacha waasi, ili wawe dhihaka kati ya adui zao, 26 ndipo Musa akasimama katika mlango wa marago, akasema, Mtu awaye yote aliye upande wa Bwana, na aje kwangu. Wana wa Lawi wote wakamkusanyikia 27 Akawaambia, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kila mtu na ajifunge upanga wake pajani mwake, akapite huko na huko toka mlango hata mlango kati ya marago, mkamchinje kila mtu ndugu yake, na kila mtu mwenziwe na kila mtu jirani yake. 28 Na hao wana wa Lawi wakafanya kama vile alivyosema Musa, wakaanguka siku ile kama watu elfu tatu. 29 Musa akasema, Jiwekeni wakfu kwa Bwana leo, naam, kila mtu juu ya mwanawe na juu ya ndugu yake; ili awape baraka leo. 30 Hata asubuhi yake Musa akawaambia watu, Mmetenda dhambi kuu; na sasa nitakwenda juu kwa Bwana, labda nitafanya upatanisho kwa ajili ya dhambi yenu. 31 Musa akarejea kwa Bwana akasema, Aa! Watu hawa wametenda dhambi kuu wamejifanyia miungu ya dhahabu. 32 Walakini sasa, ikiwa utawasamehe dhambi yao -- na kama sivyo, unifute, nakusihi, katika kitabu chako ulichoandika. 33 Bwana akamwambia Musa, Mtu ye yote aliyenitenda dhambi ndiye nitakayemfuta katika kitabu changu. 34 Basi sasa uende ukawaongoze watu hawa mpaka mahali pale ambapo nimekwambia habari zake; tazama, malaika wangu atakutangulia; pamoja na hayo siku nitakayowajilia nitawapatiliza kwa ajili ya dhambi yao. 35 Bwana akawapiga hao watu, kwa walivyoifanya ile ndama, ambayo Haruni aliifanya.

Kutoka 33

1Bwana akanena na Musa, Haya, ondokeni, katokeni hapo, wewe na hao watu uliowaleta wakwee kutoka nchi ya Misri, waende nchi hiyo niliyomwapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, niliposema, Nitakipa kizazi chako nchi hii; 2 nami nitamtuma malaika aende mbele yako; nami nitawafukuza Mkanaani, na Mwamori, na Mhiti, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi; 3 waifikilie nchi imiminikayo maziwa na asali; kwa maana mimi sitakwenda kati yenu; kwa sababu ninyi ni watu wenye shingo ngumu; nisiwaangamize ninyi katika njia. 4 Watu waliposikia habari hizo mbaya wakaomboleza wala hapana mtu aliyevaa vyombo vyake vya uzuri. 5 Bwana akamwambia Musa, Waambie wana wa Israeli, Ninyi ni watu wenye shingo ngumu; kama mimi nikiingia kati yenu dakika moja, nitawaangamiza; basi sasa vueni vyombo vyenu vya uzuri ili nipate kujua nitakalowatenda. 6 Basi wana wa Israeli wakavua vyombo vyao vyote vya uzuri, tangu mlima wa Horebu na mbele. 7 Basi desturi ya Musa, ilikuwa kuitwaa ile hema, na kuikita nje ya marago mbali na hayo marago; akaiita, hema ya kukutania. Hata kila mtu aliyekuwa akitaka neno kwa Bwana, akatoka, akaenda hata hema ya kukutania, iliyokuwa nje ya marago. 8 Hata Musa alipotoka kuiendea ile hema, watu wote waliondoka wakasimama, kila mtu mlangoni pa hema yake, akamtazama Musa, hata alipokwisha kuingia hemani. 9 Ikawa Musa alipoingia humo hemani, ile nguzo ya wingu ikashuka, ikasimama mlangoni pa ile hema; naye Bwana akasema na Musa. 10 Watu wote wakaiona nguzo ya wingu ikisimama penye mlango wa hema; watu wote wakaondoka wakasujudu, kila mtu mlangoni pa hema yake. 11 Naye Bwana akasema na Musa uso kwa uso, kama vile mtu asemavyo na rafiki yake. Kisha akageuka akarejea hata maragoni; bali mtumishi wake Yoshua, mwana wa Nuni, naye ni kijana, hakutoka mle hemani. 12 Musa akamwambia Bwana, Angalia, wewe waniambia, Wachukue watu hawa; nawe hukunijulisha ni nani utakayemtuma pamoja nami. Walakini umesema, Nakujua jina lako, nawe umepata neema mbele zangu. 13 Basi, sasa nakuomba, ikiwa nimepata neema mbele zako, unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate neema mbele zako; ukakumbuke ya kuwa taifa hilo ndilo watu wako. 14 Akasema, Uso wangu utakwenda pamoja nawe, nami nitakupa raha. 15 Naye akamwambia, Uso wako usipokwenda pamoja nami, usituchukue kutoka hapa. 16 Kwa maana itajulikanaje kuwa nimepata neema mbele zako, mimi na watu wako? Siyo kwa sababu unakwenda pamoja nasi, hata mimi na watu wako tutengwe na watu wote walio juu ya uso wa nchi? 17 Bwana akamwambia Musa, Nitafanya na neno hili ulilolinena, kwa maana umepata neema mbele zangu, nami nakujua jina lako. 18 Akasema, Nakusihi unionyeshe utukufu wako. 19 Akasema, Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la Bwana mbele yako; nami nitamfadhili yeye nitakayemfadhili; nitamrehemu yeye nitakayemrehemu. 20 Kisha akasema, Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi. 21 Bwana akasema, Tazama, hapa pana mahali karibu nami, nawe utasimama juu ya mwamba; 22 kisha itakuwa wakati unapopita utukufu wangu, nitakutia katika ufa wa ule mwamba, na kukufunika kwa mkono wangu hata nitakapokuwa nimekwisha kupita; 23 nami nitaondoa mkono wangu, nawe utaniona nyuma yangu, bali uso wangu hautaonekana.

Kutoka 34

1 Kisha Bwana akamwambia Musa, Chonga mbao mbili za mawe mfano wa zile za kwanza; nami nitaandika juu ya mbao hizo maneno hayo yaliyokuwa juu ya mbao za kwanza, hizo ulizozivunja. 2 Nawe uwe tayari asubuhi, na asubuhi ukwee juu katika mlima wa Sinai, nawe hudhurisha nafsi yako kwangu huko katika kilele cha mlima. 3 Asikwee mtu pamoja nawe, wala asionekane mtu awaye yote katika huo mlima; wala kondoo na ng'ombe wasilishe mbele ya huo mlima. 4 Naye akachonga mbao mbili za mawe mfano wa zile za kwanza; na Musa akainuka na mapema asubuhi, naye akakwea katika mlima wa Sinai, kama Bwana alivyomwamuru, akazichukua hizo mbao mbili za mawe mkononi mwake. 5 Bwana akashuka ndani ya lile wingu, akasimama pamoja naye huko, akalitangaza jina la Bwana. 6 Bwana akapita mbele yake, akatangaza, Bwana, Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; 7 mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha tatu na cha nne. 8 Musa akafanya haraka, akainamisha kichwa chake hata nchi, akasujudu. 9 Akasema, Ikiwa sasa nimepata neema mbele zako, Bwana, nakuomba, Bwana, uende kati yetu, maana ni watu wenye shingo ngumu; ukasamehe uovu wetu na dhambi yetu, ukatutwae tuwe urithi wako. 10 Akasema, Tazama, nafanya agano; mbele ya watu wangu wote nitatenda miujiza, ya namna isiyotendeka katika dunia yote, wala katika taifa lo lote; na watu wote ambao unakaa kati yao wataona kazi ya Bwana, kwa maana ni neno la kutisha nikutendalo. 11 Liangalie neno hili ninalokuamuru leo; tazama, mbele yako namtoa Mwamori, na Mkanaani, na Mhiti, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. 12 Ujihadhari nafsi yako, usije ukafanya agano na wenyeji wa nchi ile unayoiendea, lisiwe mtego katikati yako. 13 Bali utabomoa madhabahu zao, na kuvunja-vunja nguzo zao, na kuyakata-kata maashera yao. 14 Maana hutamwabudu mungu mwingine, kwa kuwa Bwana, ambaye jina lake ni mwenye wivu, ni Mungu mwenye wivu. 15 Usije ukafanya agano na wenyeji wa nchi, watu wakaenda kufanya uzinzi na miungu yao, na kuitolea sadaka miungu yao; mtu mmoja akakuita, ukaila sadaka yake. 16 Ukawaoza wana wako binti zao, nao binti zao wakaenda kufanya uzinzi na miungu yao, wakawavuta wana wenu wafanye uzinzi na miungu yao. 17 Usijifanyizie miungu ya kuyeyusha. 18 Hiyo sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu utaitunza. Utakula mikate isiyotiwa chachu muda wa siku saba, kama nilivyokuagiza, kwa majira yaliyoaganwa katika mwezi wa Abibu; kwa kuwa ulitoka Misri katika mwezi huo wa Abibu. 19 Kila kifunguacho mimba ni changu mimi; na wanyama wako wote walio waume, wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe na wa kondoo. 20 Na mzaliwa wa kwanza wa punda utamkomboa kwa mwana-kondoo; tena kwamba hutaki kumkomboa, ndipo utamvunja shingo. Wazaliwa wa kwanza wote wa wanao utawakomboa. Wala hapana atakayehudhuria mbele zangu mikono mitupu. 21 Utafanya kazi siku sita, lakini katika siku ya saba utapumzika; wakati wa kulima mashamba, na wakati wa kuvuna pia, utapumzika. 22 Nawe utaitunza sikukuu ya majuma, nayo ni ya malimbuko ya mavuno ya ngano, na sikukuu ya kukusanya vitu mwisho wa mwaka. 23 Mara tatu kila mwaka watu waume wako wote watahudhuria mbele za Bwana MUNGU, Mungu wa Israeli. 24 Kwa kuwa mimi nitazitupa nje taifa za watu mbele yako, na kuipanua mipaka yako; wala hapana mtu ye yote atakayeitamani nchi yako, hapo utakapokwea kwenda kuhudhuria mbele za Bwana Mungu wako mara tatu kila mwaka. 25 Usisongeze damu ya sadaka yangu pamoja na mkate uliotiwa chachu; wala hiyo sadaka ya sikukuu ya pasaka haitasazwa hata asubuhi. 26 Vitu vya kwanza vya malimbuko ya nchi yako utavileta na kuvitia ndani ya nyumba ya Bwana Mungu wako. Usimtokose mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake. 27 Bwana akamwambia Musa, Andika maneno haya; kwa kuwa mimi nimefanya agano nawe, na pamoja na Israeli, kwa mujibu wa maneno haya. 28 Naye alikuwa huko pamoja na Bwana siku arobaini na masiku yake; hakula chakula, wala hakunywa maji. Naye akaandika katika hizo mbao, hayo maneno ya maagano, hizo amri kumi. 29 Hata ikawa, Musa aliposhuka katika mlima Sinai, na zile mbao mbili za ushuhuda zilikuwa mkononi mwa Musa, hapo aliposhuka katika mlima, Musa hakujua ya kuwa ngozi ya uso wake iling'aa kwa sababu amesema naye. 30 Basi Haruni na wana wote wa Israeli walipomwona Musa, tazama, ngozi ya uso wake iling'aa; nao wakaogopa kumkaribia. 31 Musa akawaita; Haruni na wakuu wote wa kusanyiko wakarudi kwake; Musa akasema nao. 32 Baadaye wana wa Israeli wote wakakaribia; akawausia maneno yote ambayo Bwana amemwambia katika mlima Sinai. 33 Na Musa alipokuwa amekwisha kusema nao, akatia utaji juu ya uso wake. 34 Lakini desturi ya Musa ilikuwa alipoingia mbele za Bwana kusema naye, kuuvua huo utaji mpaka atoke; akatoka akawaambia wana wa Israeli maneno yote aliyoambiwa. 35 Wana wa Israeli wakauona uso wa Musa ya kuwa ngozi ya uso wake Musa iling'aa; naye Musa akautia utaji juu ya uso wake tena, hata alipoingia kusema naye.

Kutoka 35

1 Musa akakutanisha mkutano wote wa wana wa Israeli, na kuwaambia, Maneno aliyoyausia Bwana ni haya, kwamba myafanye. 2 Fanyeni kazi siku sita, lakini siku ya saba itakuwa siku takatifu kwenu; ni Sabato ya kustarehe kabisa kwa Bwana; mtu awaye yote atakayefanya kazi yo yote katika siku hiyo atauawa. 3 Hamtawasha moto katika nyumba zenu kwa siku ya Sabato. 4 Kisha Musa akanena na mkutano wote wa wana wa Israeli, akawaambia, Neno hili ndilo aliloliamuru Bwana, akisema, 5 Katwaeni kati yenu matoleo kwa Bwana; mtu awaye yote aliye na moyo wa kupenda, ayalete matoleo; dhahabu na fedha na shaba; 6 na nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na kitani nzuri, na singa za mbuzi; 7 na ngozi za kondoo waume zilizotiwa rangi nyekundu, na ngozi za pomboo, na mbao za mshita; 8 na mafuta kwa hiyo taa, na viungo vya manukato kwa hayo mafuta ya kutiwa, na kwa huo uvumba mzuri; 9 na vito vya shohamu, na vito vya kutiwa kwa hiyo naivera, na kwa hicho kifuko cha kifuani. 10 Na kila mtu kati yenu aliye na moyo wa hekima na aje, na kuyafanya hayo yote ambayo Bwana ameyaagiza; 11 yaani, hiyo maskani na hema yake, na kifuniko chake, na vifungo vyake, na mbao zake, na mataruma yake, na viguzo vyake, na matako yake; 12 hilo sanduku, na miti yake, na hicho kiti cha rehema, na lile pazia la sitara; 13 na hiyo meza, na miti yake, na vyombo vyake vyote, na hiyo mikate ya wonyesho; 14 na hicho kinara cha taa kwa mwanga, na vyombo vyake, na taa zake, na hayo mafuta kwa nuru; 15 na hiyo madhabahu ya kufukizia uvumba, na miti yake, na hayo mafuta ya kupaka, na huo uvumba mzuri, na hicho kisitiri cha mlango, mlangoni mwa hiyo maskani; 16 na hiyo madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, pamoja na wavu wake wa shaba, na miti yake, na vyombo vyake vyote, na hilo birika na tako lake; 17 na hizo kuta za nguo za ua, na viguzo vyake, na matako yake, na pazia la lango la ua; 18 na vile vigingi vya maskani, na vigingi vya ua, na kamba zake 19 na mavazi yenye kufumwa kwa uzuri, kwa ajili ya kutumika ndani ya mahali patakatifu, hayo mavazi matakatifu ya Haruni kuhani, na mavazi ya wanawe, ili kutumika katika kazi ya ukuhani. 20 Basi mkutano wote wa wana wa Israeli wakaondoka hapo mbele ya Musa. 21 Wakaja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza, na kila mtu ambaye roho yake ilimfanya kuwa apenda, nao wakaleta sadaka za kumpa Bwana, kwa kazi ya hema ya kukutania, na kwa utumishi wake, na kwa hayo mavazi matakatifu. 22 Nao wakaja, waume kwa wake, wote waliokuwa na moyo wa kupenda, wakaleta vipini, na hazama, na pete za muhuri, na vikuku, na vyombo vyote vya dhahabu; kila mtu aliyetoa toleo la dhahabu la kumpa Bwana. 23 Tena kila mtu aliyeona kwake nyuzi za rangi ya samawi, na nyuzi za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri, na singa za mbuzi, na ngozi za kondoo waume zilizotiwa rangi nyekundu, na ngozi za pomboo, akavileta. 24 Kila mtu aliyetoa toleo la fedha, na la shaba, akaileta sadaka ya Bwana; na kila mtu, aliyeona kwake mti wa mshita kwa kazi yo yote ya huo utumishi, akauleta. 25 Na wanawake wote waliokuwa na mioyo ya hekima, walisokota kwa mikono yao, nao wakaleta hizo walizokuwa wamezisokota, nguo za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na hizo nyuzi nyekundu, na hiyo nguo ya kitani nzuri. 26 Na wanawake wote ambao mioyo yao iliwahimiza katika hekima wakasokota hizo singa za mbuzi. 27 Na hao wakuu wakavileta vile vito vya shohamu, na vito vya kutiwa, kwa hiyo naivera, na kwa hicho kifuko cha kifuani, 28 na viungo vya manukato, na mafuta; kwa hiyo taa, na kwa hayo mafuta ya kutiwa, na kwa huo uvumba mzuri. 29 Wana wa Israeli wakaleta sadaka za kumpa Bwana kwa moyo wa kupenda; wote, waume kwa wake, ambao mioyo yao iliwafanya kuwa wapenda kuleta kwa hiyo kazi, ambayo Bwana aliamuru ifanywe kwa mkono wa Musa. 30 Kisha Musa akawaambia wana wa Israeli, Angalieni, Bwana amemwita kwa jina lake Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda; 31 naye amemjaza roho ya Mungu, katika hekima, na akili, na ujuzi, na kazi ya ustadi kila aina; 32 na kuvumbua kazi za werevu, na kufanya kazi ya dhahabu, na fedha, na shaba, 33 na kukata vito vya kutilia, na kuchora miti, atumike katika kazi za werevu kila aina. 34 Naye amemtilia moyoni mwake ili apate kufundisha, yeye, na Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani. 35 Amewajaza watu hao akili za moyoni, ili watumike katika kazi kila aina, ya mwenye kuchora mawe, na kazi ya werevu, na ya mwenye kutia taraza, katika nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri, na ya mwenye kufuma nguo; ya hao wafanyao kazi yo yote, na ya wenye kuvumbua kazi za werevu.

Kutoka 36

1 Basi Bezaleli na Oholiabu watatenda kazi, na kila mtu mwenye moyo wa hekima, ambaye Bwana amemtia akili na hekima ili ajue kufanya kazi hiyo yote kwa huo utumishi wa mahali patakatifu, kama hayo yote Bwana aliyoyaagiza. 2 Basi Musa akawaita Bezaleli na Oholiabu, na kila mtu aliyekuwa na moyo wa akili, ambaye Bwana alimtia moyoni mwake hekima, kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza ili aende kuifanya kazi hiyo; 3 nao wakapokea mkononi mwa Musa matoleo yote, ambayo hao wana wa Israeli walikuwa wameyaleta kwa ajili ya huo utumishi wa mahali patakatifu, ili wapafanye. Kisha wakamletea matoleo kila siku asubuhi kwa moyo wa kupenda. 4 Na hao watu wote wenye hekima, waliotumika katika kazi yote ya mahali patakatifu, wakaenda kila mtu kutoka katika kazi yake aliyokuwa akiifanya; 5 nao wakasema na Musa, na kumwambia, Watu waleta vitu vingi sana zaidi ya hivyo vitoshavyo kwa ajili ya utumishi wa hiyo kazi, ambayo Bwana aliagiza ifanywe. 6 Basi Musa akatoa amri, nao wakatangaza mbiu katika marago yote, wakisema, Wasifanye kazi tena, mtu mume wala mwanamke, kwa ajili ya matoleo kwa mahali patakatifu. Basi watu wakazuiwa wasilete tena. 7 Kwani vile vitu walivyokuwa navyo vilikuwa vyatosha kwa kuifanya kazi hiyo yote, kisha vilizidi. 8 Basi kila mtu mwenye moyo wa hekima miongoni mwa hao waliofanya kazi, akaifanya hiyo maskani ya mapazia kumi; ya nguo ya kitani nzuri ya kusokotwa, na nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu; pamoja na makerubi, kazi ya fundi stadi; ndivyo alivyoyafanya. 9 Urefu wa kila pazia ulikuwa ni dhiraa ishirini na nane, na upana wa kila pazia ulikuwa ni dhiraa nne; mapazia yote yalikuwa ya kipimo kimoja. 10 Naye akaunganisha mapazia matano hili na hili; na mapazia matano mengine akayaunganisha hili na hili. 11 Kisha akafanya matanzi ya rangi ya samawi katika ncha za pazia moja, katika upindo wa kiungo chake; akafanya vivyo katika ncha ya pazia lililokuwa upande wa nje katika kiungo cha pili. 12 Akafanya matanzi hamsini katika pazia moja, na matanzi hamsini katika upindo wa pazia lililokuwa katika kiungo cha pili; hayo matanzi yalikuwa yakabiliana hili na hili. 13 Kisha akafanya vifungo hamsini vya dhahabu, na kuyaunganya hayo mapazia hili na hili kwa vile vifungo; hivi ile maskani ilikuwa ni moja. 14 Kisha akafanya vifuniko vya singa za mbuzi kuwa hema ya kuifunika hiyo maskani; akafanya mapazia kumi na moja. 15 Urefu wa kila pazia ulikuwa ni dhiraa thelathini, na upana wa kila pazia ulikuwa ni dhiraa nne; hayo mapazia yote kumi na moja yalikuwa ya kipimo kimoja. 16 Naye akaunganya mapazia matano mbali, na mapazia sita mbali. 17 Kisha akafanya matanzi hamsini katika upindo wa pazia lililo upande wa nje katika kile kiungo, naye akafanya matanzi hamsini katika ncha ya pazia lililokuwa upande wa nje katika kiungo cha pili. 18 Kisha akafanya vifungo hamsini vya shaba aiunganye ile hema pamoja, ili iwe hema moja. 19 Kisha akafanya kifuniko kwa ajili ya hiyo hema cha ngozi za kondoo waume zilizotiwa rangi nyekundu; tena juu yake akafanya kifuniko cha ngozi za pomboo. 20 Kisha akafanya mbao za mti wa mshita kwa hiyo maskani, zilizosimama. 21 Urefu wa kila ubao ulikuwa ni dhiraa kumi, na upana wa kila ubao ulikuwa ni dhiraa moja na nusu. 22 Kila ubao ulikuwa na ndimi mbili, zilizounganywa pamoja; ndivyo alivyozifanya hizo mbao zote za maskani. 23 Naye akazifanya hizo mbao kwa ajili ya hiyo maskani; mbao ishirini kwa upande wa kusini kuelekea kusini; 24 naye akafanya matako ya fedha arobaini yawe chini ya hizo mbao ishirini; matako mawili chini ya ubao mmoja kwa hizo ndimi zake mbili, na matako mawili chini ya ubao mwingine kwa ndimi zake mbili. 25 Na kwa upande wa pili wa maskani upande wa kaskazini, akafanya mbao ishirini, 26 na matako yake ya fedha arobaini; matako mawili chini ya ubao mmoja, na matako mawili chini ya ubao mwingine. 27 Na kwa upande wa nyuma wa hiyo maskani kuelekea magharibi akafanya mbao sita. 28 Naye akafanya mbao mbili kwa pembe za maskani upande wa nyuma. 29 Nazo zilikuwa mbao pacha upande wa chini, vivyo zilishikamana pamoja hata ncha ya juu kufikilia pete ya kwanza; ndivyo alivyofanya zote mbili katika hizo pembe mbili. 30 Hivyo zilikuwa mbao nane, na matako yake ya fedha, matako kumi na sita, matako mawili chini ya kila ubao. 31 Kisha akafanya mataruma ya miti ya mshita; matano kwa mbao za upande mmoja wa maskani; 32 na mataruma matano kwa mbao za upande wa pili wa maskani, na mataruma matano kwa hizo mbao za maskani zilizokuwa upande wa nyuma kuelekea magharibi. 33 Naye akalifanya hilo taruma la katikati lipenye kati ya hizo mbao kutoka upande huu hata upande huu. 34 Naye akazifunika hizo mbao dhahabu, akazifanya zile pete zake za dhahabu ziwe mahali pa hayo mataruma, akayafunika dhahabu hayo mataruma. 35 Kisha akafanya hilo pazia la nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri zilizosokotwa; akatia na makerubi kazi ya fundi stadi, ndivyo alivyofanya. 36 Naye akafanya kwa ajili yake nguzo nne za mti wa mshita, akazifunika dhahabu; na kulabu zake zilikuwa za dhahabu; naye akasubu kwa ajili yake matako manne ya fedha. 37 Kisha akafanya pazia la sitara kwa ajili ya mlango wa Hema, la nguo ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na nyekundu, na nguo ya kitani nzuri ya kusokotwa, kazi ya mwenye kutia taraza, 38 na nguzo zake tano pamoja na kulabu zake; naye akavifunika dhahabu vichwa vyake na vifungo vyake; na matako yake matano yalikuwa ya shaba.

Kutoka 37

1 Kisha Bezaleli akalifanya lile sanduku la mti wa mshita, urefu wake ulikuwa dhiraa mbili na nusu, na upana wake ulikuwa dhiraa moja na nusu, na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa moja na nusu; 2 akalifunika dhahabu safi, ndani na nje, akafanya na ukingo wa dhahabu kulizunguka pande zote. 3 Naye akasubu pete nne za dhahabu kwa ajili yake, katika miguu yake minne; pete mbili upande wake mmoja na pete mbili upande wake wa pili. 4 Akafanya na miti ya kulichukulia, ya mti wa mshita akaifunika dhahabu. 5 Naye akaitia hiyo miti katika zile pete zilizokuwa ubavuni mwa sanduku, ili kulichukua hilo sanduku. 6 Kisha akafanya kiti cha rehema cha dhahabu safi; urefu wake ulikuwa dhiraa mbili na nusu na upana wake ulikuwa dhiraa moja na nusu. 7 Kisha akafanya makerubi mawili ya dhahabu; akayafanya ya kazi ya kufua, yawe katika miisho miwili ya kiti cha rehema; 8 kerubi moja mwisho huu, na kerubi moja mwisho huu; alifanya hayo makerubi mawili ya kitu kimoja na hicho kiti cha rehema katika miisho yake miwili. 9 Na hayo makerubi yakayanyosha mabawa yao juu, na kukifunika hicho kiti cha rehema kwa mabawa yao, na nyuso zao zilikuwa zaelekeana hili na hili; nyuso za hayo makerubi zilikuwa zikielekea kiti cha rehema. 10 Kisha akafanya hiyo meza ya mti wa mshita; urefu wake ulikuwa ni dhiraa mbili, na upana wake ulikuwa ni dhiraa moja, na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa moja na nusu; 11 naye akaifunika dhahabu safi, akaifanyia ukingo wa dhahabu kuizunguka pande zote. 12 Kisha akaifanyia upapi wa upana wa shibiri kuizunguka pande zote, akauzungushia ukingo wa urembo wa dhahabu ule upapi. 13 Naye akasubu vikuku vinne vya dhahabu kwa ajili yake, akavitia vile vikuku katika pembe nne, katika miguu yake minne. 14 Vile vikuku vilikuwa karibu na ule upapi, ili viwe mahali pa kutilia ile miti, ya kuichukulia meza. 15 Naye akaifanya hiyo miti ya kuichukulia, ya mti wa mshita, akaifunika dhahabu, ili kuichukua hiyo meza. 16 Kisha, vile vyombo vilivyokuwa juu ya meza, sahani zake, na miiko yake, na bakuli zake, na makopo yake ya kumiminia, akavifanya vya dhahabu safi. 17 Kisha akakifanya kile kinara cha taa cha dhahabu safi, akakifanya kile kinara cha taa cha kazi ya kufua, tako lake, na mti wake; vikombe vyake, na matovu yake, na maua yake, vyote vilikuwa vya kitu kimoja nacho, 18 nacho kilikuwa na matawi sita yaliyotoka ubavuni mwake; matawi matatu ya kinara yalikuwa upande huu, na matawi matatu ya kinara yalikuwa upande huu; 19 vikombe vitatu, vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi vilikuwa katika tawi moja, tovu na ua; na vikombe vitatu, vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi, katika tawi la pili, tovu na ua; yalikuwa ni vivyo hivyo yale matawi sita yaliyokuwa katika hicho kinara. 20 Katika kinara mlikuwa na vikombe vinne, vilivyofanywa mfano wa maua ya mlozi, matovu yake na maua yake; 21 kisha chini ya matawi mawili mlikuwa na tovu iliyokuwa ya kitu kimoja nacho, na chini ya matawi mawili mengine mlikuwa na tovu ya kitu kimoja nacho, tena chini ya matawi mawili hayo mengine mlikuwa na tovu ya kitu kimoja nacho; kwa ajili ya hayo matawi sita, yaliyotokana nacho. 22 Hayo matovu yake na matawi yake yalikuwa ya kitu kimoja nacho; kinara hicho kizima chote pia ni kazi moja ya kufua ya dhahabu safi. 23 Kisha akafanya taa zake saba, na makoleo yake, na visahani vyake, vya dhahabu safi. 24 Akakifanya cha talanta moja ya dhahabu safi, pamoja na vyombo vyake vyote. 25 Kisha akafanya hiyo madhabahu ya kufukizia uvumba ya mti wa mshita; urefu wake ulikuwa ni dhiraa moja, na upana wake ulikuwa ni dhiraa moja, ilikuwa mraba; na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa mbili; na pembe zake zilikuwa za kitu kimoja nayo. 26 Naye akaifunika dhahabu safi, upande wa juu, na mbavu zake pande zote, na hizo pembe zake; akaifanyia na ukingo wa dhahabu kuizunguka pande zote. 27 Naye akaifanyia vikuku viwili vya dhahabu na kuvitia chini ya ukingo wake, katika mbavu zake mbili, katika pande zake mbili, viwe ni mahali pa hiyo miti ya kuichukulia. 28 Kisha akafanya hiyo miti kwa mti wa mshita, na kuifunika dhahabu. 29 Kisha akayafanya hayo mafuta matakatifu ya kutiwa, na ule uvumba safi wa viungo vya manukato vizuri, kwa kuandama kazi ya mtengezaji manukato.

Kutoka 38

1 Kisha akafanya hiyo madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, ya mti wa mshita urefu wake ulikuwa dhiraa tano, na upana wake ulikuwa dhiraa tano, ilikuwa mraba; na kwenda juu kwake kulikuwa dhiraa tatu. 2 Naye akazifanya pembe zake katika ncha zake nne; hizo pembe zilikuwa za kitu kimoja nayo; naye akaifunika shaba. 3 Kisha akafanya vyombo vyote vya madhabahu, yaani sufuria zake, na majembe yake, na mabakuli yake, na uma zake, na meko yake; vyombo vyake vyote akavifanya vya shaba. 4 Naye akaifanyia madhabahu wavu wa shaba, akautia chini ya ukingo kuizunguka pande zote, ukawa katikati ya hiyo madhabahu. 5 Naye akasubu vikuku vinne kwa kutiwa katika pembe nne za huo wavu wa shaba, viwe mahali pa kutia ile miti ya kuichukulia. 6 Naye akaifanya hiyo miti kwa mti wa mshita na kuifunika shaba. 7 Naye akaitia ile miti katika vile vikuku vilivyokuwa katika mbavu za hiyo madhabahu, ili kuichukua; akaifanya yenye mvungu ndani, kwa zile mbao. 8 Kisha akafanya hilo birika la shaba, na tako lake la shaba; shaba hiyo ilikuwa ni ya vioo vya wanawake wenye kutumika, waliokuwa wakitumika mlangoni mwa hema ya kukutania. 9 Naye akafanya ule ua; upande wa kusini kwa kuelekea kusini, chandarua ya ua ilikuwa ya nguo ya kitani nzuri ya kusokotwa, kiasi cha dhiraa mia; 10 nguzo zake zilikuwa ishirini, na matako yake yalikuwa ishirini, yalikuwa ya shaba; kulabu za nguzo na vitanzi vyake vilikuwa vya fedha. 11 Upande wa kaskazini ulikuwa ni dhiraa mia vivyo, nguzo zake ishirini na matako yake ishirini, yalikuwa ni ya shaba; kulabu za nguzo na vitanzi vyake vilikuwa vya fedha. 12 Upande wa magharibi mlikuwa na chandarua ya dhiraa hamsini, nguzo zake zilikuwa ni kumi, na matako yake kumi; kulabu za hizo nguzo na vitanzi vyake vilikuwa vya fedha. 13 Upande wa mashariki kuelekea mashariki dhiraa hamsini. 14 Chandarua ya upande mmoja wa lango ilikuwa dhiraa kumi na tano urefu wake; na nguzo zake tatu, na matako yake matatu; 15 ni vivyo upande wa pili; upande huu na huu langoni mwa ua mlikuwa na chandarua ya dhiraa kumi na tano urefu wake; nguzo zake zilikuwa ni tatu, na matako yake matatu. 16 Chandarua za nguo zote za ule ua zilizouzunguka pande zote zilikuwa za nguo ya kitani nzuri iliyosokotwa. 17 Na matako ya zile nguzo yalikuwa ya shaba; kulabu za hizo nguzo na vitanzi vyake vilikuwa vya fedha; na vichwa vya zile nguzo vilikuwa ni vya fedha; na nguzo zote za huo ua ziliungwa kwa vitanzi vya fedha. 18 Na hilo pazia la lango la ua, lilikuwa ni kazi ya mwenye kutia taraza, lilikuwa la nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri ya kusokotwa; lilikuwa na urefu wake dhiraa ishirini, na kutukuka kwake katika huo upana wake kulikuwa dhiraa tano, kupatana na ile chandarua ya ua. 19 Na nguzo zake zilikuwa nne, na matako yake manne, yalikuwa ya shaba; kulabu zake zilikuwa za fedha, na vichwa vyake na vitanzi vyake vilikuwa vya fedha. 20 Na vigungi vyote vya maskani, na vya ua ulioizunguka pande zote vilikuwa vya shaba. 21 Jumla ya vile vyombo vilivyofanywa kwa ajili ya hiyo maskani, hiyo maskani ya ushuhuda ni hii, kama vilivyohesabiwa, kama maagizo ya Musa yalivyokuwa, kwa ajili ya utumishi wa Walawi kwa mkono wa Ithamari, mwana wa Haruni, kuhani. 22 Na Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda, akafanya yote Bwana aliyomwagiza Musa. 23 Na pamoja naye alikuwa na Oholiabu, mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani, aliyekuwa fundi wa kuchora nakshi, mfanyaji wa kazi mwerevu, naye alikuwa mwenye kutia taraza za nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri. 24 Dhahabu yote iliyotumiwa kwa ajili ya hiyo kazi, katika kazi hiyo yote ya mahali patakatifu, hiyo dhahabu ya matoleo, ilikuwa ni talanta ishirini na kenda, na shekeli mia saba na thelathini, kwa kadiri ya shekeli ya mahali patakatifu. 25 Na fedha ya hao waliohesabiwa, watu wa huo mkutano ilikuwa talanta mia, na shekeli elfu moja na mia saba na sabini na tano kwa kadiri ya shekeli ya mahali patakatifu; 26 kichwa beka, maana, nusu shekeli, kwa kadiri ya shekeli ya mahali patakatifu, kwa ajili ya kila mtu aliyepita kwa wale waliohesabiwa, aliyekuwa wa umri wa miaka ishirini au zaidi, kwa ajili ya watu waume sita mia na tatu elfu, na mia tano na hamsini (603,550). 27 Na hizo talanta mia za fedha zilikuwa kwa kusubu yale matako ya mahali patakatifu na matako ya hilo pazia; matako mia kwa hizo talanta mia, talanta moja tako moja. 28 Na kwa hizo shekeli elfu moja na mia saba, na sabini na tano, akafanya vifungo vya hizo nguzo, na kuvifunika fedha vile vichwa vyake, na kufanya vitanzi vyake. 29 Na hiyo shaba iliyoletwa ilikuwa ni talanta sabini, na shekeli elfu mbili na mia nne. 30 Naye akafanya ya hiyo shaba matako kwa ajili ya lango la hema ya kukutania, na hiyo madhabahu ya shaba, na ule wavu wa shaba kwa ajili yake na vyombo vyote vya hiyo madhabahu, 31 na matako ya ua kuuzunguka pande zote, na matako ya lango la huo ua, na vigingi vyote vya maskani, na vigingi vyote vya huo ua uliozunguka pande zote.

Kutoka 39

1 Na zile nyuzi za rangi ya samawi, na nyuzi za rangi ya zambarau, na nyekundu, wakafanya mavazi yaliyofumwa kwa ustadi sana kwa ajili ya kutumika katika mahali patakatifu, na kuyafanya hayo mavazi matakatifu ya Haruni, vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 2 Naye akaifanya hiyo naivera, ya nyuzi za dhahabu, na za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na kitani nzuri ya kusokotwa. 3 Nao wakaifua hiyo dhahabu hata ikawa mabamba membamba sana, kisha wakaikata iwe nyuzi, ili wapate kuifuma pamoja na hizo nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyuzi nyekundu na za kitani nzuri, kazi ya fundi stadi sana. 4 Nao wakafanya na vipande vya mabegani kwa ajili yake, vilivyoungwa pamoja; viliungwa pamoja kwa ncha zake mbili. 5 Na huo mshipi wa kazi ya werevu, uliokuwa juu yake ili kuifunga mahali pake; ulikuwa wa kitu kimoja, na wa kazi moja na naivera ya dhahabu, na rangi ya samawi, na rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri ya kusokotwa; vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 6 Nao wakavitengeza vile vito vya shohamu, vilivyotiwa katika vijalizo vya dhahabu, vilivyochorwa mfano wa kuchora kwake muhuri, kwa majina ya hao wana wa Israeli. 7 Naye akavitia katika vile vipande vya mabegani vya hiyo naivera, viwe vito vya ukumbusho kwa wana wa Israeli, kama Bwana alivyomwagiza Musa. 8 Naye akafanya kile kifuko cha kifuani, kazi ya fundi stadi, kama hiyo kazi ya naivera; ya nyuzi za dhahabu, na za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri ya kusokotwa. 9 Kilikuwa mraba; wakakifanya kile kifuko cha kifuani kwa kukikunja; urefu wake ulikuwa shibiri, na upana wake ulikuwa shibiri, tena kilikuwa ni cha kukunjwa. 10 Nao wakatia safu nne za vito ndani yake, safu moja ilikuwa ni akiki, na yakuti ya rangi ya manjano, na baharamani, vilikuwa ni safu ya kwanza. 11 Na safu ya pili ilikuwa zumaridi, na yakuti samawi, na almasi. 12 Na safu ya tatu ilikuwa ni hiakintho, na akiki nyekundu, na amethisto. 13 Na safu ya nne ilikuwa ni zabarajadi, na shohamu, na yaspi: vito hivyo vilikuwa vimetiwa katika vijalizo vya dhahabu, kila kimoja mahali pake. 14 Na hivyo vito vilikuwa vyaandama majina ya wana wa Israeli, kumi na mawili, sawasawa na majina yao; mfano wa kuchora muhuri, kila moja kwa jina lake, kwa zile kabila kumi na mbili. 15 Nao wakafanya katika kile kifuko cha kifuani mikufu mfano wa kamba, ya kazi ya kusokotwa ya dhahabu safi. 16 Nao wakafanya vijalizo viwili vya dhahabu, na pete mbili za dhahabu; nao wakazitia hizo pete mbili katika ncha mbili za hicho kifuko. 17 Nao wakaitia hiyo mikufu miwili iliyosokotwa katika hizo pete mbili zilizokuwa katika ncha mbili za hicho kifuko. 18 Na ncha hizo mbili nyingine, za hiyo mikufu miwili ya kusokotwa, wakazitia katika vile vijalizo viwili, na kuvitia katika vile vipande vya mabegani vya naivera, upande wa mbele. 19 Nao wakafanya pete mbili za dhahabu, na kuzitia katika ncha mbili za kifuko cha kifuani, katika ukingo wake, ulio upande wa naivera ulio ndani. 20 Nao wakafanya pete mbili za dhahabu, na kuzitia katika vile vipande viwili vya ile naivera chini yake, upande wa mbele, karibu na kifungo chake, juu ya huo mshipi wa naivera uliosukwa kwa ustadi. 21 Nao wakakikaza kile kifuko kwa pete zake kwenye naivera kwa ukanda wa rangi ya samawi, ili kikae pale juu ya mshipi wa naivera uliosukwa kwa ustadi, na ya kwamba kifuko cha kifuani kisiachane na naivera; vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 22 Naye akafanya hiyo joho ya naivera ya kazi ya kusuka, rangi ya samawi yote; 23 na hilo tundu lililokuwa katikati yake, mfano wa tundu lililo katika kanzu ya chuma, na utepe wake kulizunguka hilo tundu, ili lisipasuke. 24 Nao wakatia katika upindo wa joho makomamanga ya nyuzi za rangi ya samawi, na rangi ya zambarau, na rangi nyekundu, na kitani iliyosokotwa. 25 Nao wakafanya njuga za dhahabu safi, na kuzitia hizo njuga kati ya hayo makomamanga pande zote, kati ya hayo makomamanga; 26 njuga na komamanga, njuga na komamanga katika pindo za joho kuizunguka pande zote, ili kutumika kwa hiyo; vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 27 Nao wakafanya hizo kanzu za nguo ya kitani nzuri ya kufumwa, kwa Haruni, na kwa wanawe 28 na hicho kilemba cha nguo ya kitani nzuri, na zile kofia nzuri za kitani, na hizo suruali za nguo ya kitani nzuri iliyosokotwa, 29 na huo mshipi wa nguo nzuri ya kitani iliyosokotwa, na rangi ya samawi, na rangi ya zambarau, na nyekundu, kazi ya fundi mwenye kutia taraza; vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 30 Nao wakafanya hilo bamba la hiyo taji takatifu la dhahabu safi, na kuandika juu yake andiko, mfano wa kuchorwa kwa muhuri, MTAKATIFU KWA Bwana. 31 Nao wakatia ukanda wa rangi ya samawi ili kulifunga katika hicho kilemba upande wa juu; vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 32 Basi ndivyo ilivyomalizwa kazi yote ya maskani ya hema ya kukutania; na wana wa Israeli walifanya kama yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyofanya. 33 Nao wakamletea Musa hiyo maskani; yaani Hema, na vyombo vyake vyote, vifungo vyake, na mbao zake, na mataruma yake, na nguzo zake, na matako yake; 34 na kifuniko chake cha ngozi za kondoo waume zilizotiwa rangi nyekundu, na kifuniko cha ngozi za pomboo, na pazia la sitara; 35 na sanduku la ushuhuda, na miti yake, na kiti cha rehema; 36 na meza, na vyombo vyake vyote, na mikate ya wonyesho; 37 na kinara cha taa safi, na taa zake, hizo taa za kuwekwa mahali pake, na vyombo vyake vyote, na mafuta ya taa, 38 na madhabahu ya dhahabu, na mafuta ya kutiwa, na uvumba mzuri, na pazia kwa mlango wa hema; 39 na madhabahu ya shaba, na wavu wake wa shaba, na miti yake, na vyombo vyake vyote, na birika na tako lake; 40 na ukuta wa nguo wa ua, na nguzo zake na matako yake, na pazia la lango la ua, na kamba zake, na vigingi vyake, na vyombo vyote vya kutumiwa katika utumishi wa maskani, kwa hiyo hema ya kukutania, 41 na mavazi ya kazi nzuri kwa utumishi katika mahali patakatifu, na mavazi matakatifu ya Haruni kuhani, na mavazi ya wanawe, ili kutumika katika kazi ya ukuhani. 42 Sawasawa na yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyoifanya hiyo kazi yote wana wa Israeli. 43 Musa akaiona hiyo kazi yote, na tazama, walikuwa wameimaliza; vile vile kama Bwana alivyoagiza, walikuwa wameifanya vivyo; basi Musa akawaombea heri.

Kutoka 40

1 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza utaisimamisha hiyo maskani ya hema ya kukutania. 3 Nawe utatia ndani yake sanduku la ushuhuda, nawe utalisitiri hilo sanduku kwa pazia. 4 Nawe utaleta meza na kuitia ndani, na kuviweka sawasawa vile vitu juu yake; kisha utakileta ndani kile kinara cha taa, na kuziwasha taa zake. 5 Kisha utaisimamisha madhabahu ya dhahabu kwa kufukizia uvumba mbele ya sanduku la ushuhuda, na kulitia pazia mlangoni mwa hiyo maskani. 6 Kisha utaweka madhabahu ya kuteketeza sadaka mbele ya mlango wa maskani ya hema ya kukutania. 7 Kisha utaliweka birika kati ya hema ya kukutania na hiyo madhabahu, nawe utatia maji ndani yake. 8 Kisha utausimamisha ukuta wa ua kuuzunguka pande zote, na kuitundika sitara ya lango la ua. 9 Kisha utayatwaa mafuta ya kutiwa, na kuitia mafuta hiyo maskani, na kila kitu kilicho ndani yake, na kuiweka iwe takatifu, na vyombo vyake vyote; nayo itakuwa takatifu. 10 Kisha utaitia mafuta madhabahu ya kuteketeza sadaka, na vyombo vyake vyote; na kuiweka takatifu madhabahu; na hiyo madhabahu itakuwa takatifu sana. 11 Kisha utalitia mafuta birika na tako lake, na kuliweka liwe takatifu. 12 Kisha utamleta Haruni na wanawe hapo mlangoni pa hema ya kukutania, nawe utawaosha kwa maji. 13 Kisha utamvika Haruni mavazi matakatifu; nawe utamtia mafuta, na kumweka awe mtakatifu, ili apate kunitumikia katika kazi ya ukuhani. 14 Kisha utawaleta wanawe, na kuwavika kanzu zao; 15 nawe utawatia mafuta kama ulivyomtia mafuta baba yao, ili wanitumikie katika kazi ya ukuhani; na huko kutiwa mafuta kwao kutakuwa ni kwa ukuhani wa milele katika vizazi vyao vyote. 16 Musa akafanya hayo yote; kama yote Bwana aliyoagiza ndivyo alivyofanya. 17 Hata mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili, siku ya kwanza ya mwezi ile maskani ilisimamishwa. 18 Musa akaisimamisha maskani, akayaweka matako yake, akazisimamisha mbao zake akayatia mataruma yake, akazisimamisha nguzo zake. 19 Akaitanda hema juu ya maskani, akakitia kifuniko cha hema juu yake; kama Bwana alivyomwamuru Musa. 20 Akautwaa ule ushuhuda, akautia ndani ya sanduku, akaiweka miti ya kuchukulia juu ya sanduku, akakiweka kiti cha rehema juu ya sanduku; 21 kisha akalileta sanduku akalitia ndani ya maskani, naye akalitundika pazia la sitara, akalisitiri sanduku la ushuhuda; kama Bwana alivyomwamuru Musa. 22 Akaitia meza ndani ya hema ya kukutania, upande wa maskani ulioelekea kaskazini, nje ya pazia. 23 Akaipanga ile mikate juu yake mbele za Bwana; kama Bwana alivyomwamuru Musa. 24 Kisha akakitia kinara cha taa ndani ya hema ya kukutania, kuikabili ile meza, upande wa maskani ulioelekea kusini. 25 Kisha akaziwasha taa zake mbele za Bwana, kama Bwana alivyomwamuru Musa. 26 Akaitia madhabahu ya dhahabu ndani ya hema ya kukutania mbele ya pazia. 27 Akafukiza juu yake uvumba wa manukato kama Bwana alivyomwamuru Musa. 28 Akalitia pazia la mlango wa maskani. 29 Akaiweka madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa mlangoni pa maskani ya kukutania, akatoa sadaka ya kuteketezwa juu yake, na sadaka ya unga; kama Bwana alivyomwamuru Musa. 30 Akaliweka birika kati ya hema ya kukutania na madhabahu, akatia maji ndani yake ya kuoshea. 31 Musa na Haruni, na wanawe wakanawa mikono yao na miguu yao ndani yake; 32 hapo walipoingia hema ya kukutania, na hapo walipoikaribia madhabahu walinawa kama Bwana alivyomwamuru Musa. 33 Akausimamisha ukuta wa ua kuizunguka maskani na madhabahu, akalitundika pazia la mlango wa ule ua. Basi Musa akaimaliza hiyo kazi. 34 Ndipo lile wingu likaifunikiza hema ya kukutania, na huo utukufu wa Bwana ukaijaza maskani. 35 Wala Musa hakuweza kuliingia hema la kukutania, kwa sababu lile wingu lilikaa juu yake, na huo utukufu wa Bwana ukaijaza maskani. 36 Na hapo lile wingu lilipoinuliwa kutoka juu ya maskani, wana wa Israeli wakaenda mbele katika safari zao zote, 37 bali kama lile wingu halikuinuliwa, wakati ule hawakusafiri hata siku ile lilipoinuliwa tena. 38 Kwa maana lile wingu la Bwana lilikuwa juu ya maskani wakati wa mchana, na mlikuwa na moto ndani yake wakati wa usiku, mbele ya macho ya nyumba ya Israeli katika safari zao zote.

Mambo ya Walawi 1

1 Bwana akamwita Musa, na kusema naye kutoka katika hema ya kukutania, akamwambia, 2 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtu wa kwenu atakapomtolea Bwana matoleo, mtatoa matoleo yenu katika wanyama wa mifugo, katika ng'ombe na katika kondoo. 3 Matoleo yake kwamba ni sadaka ya kuteketezwa ya ng'ombe, atatoa ng'ombe mume mkamilifu; ataleta mlangoni pa hema ya kukutania, ili akubaliwe mbele ya Bwana. 4 Kisha ataweka mkono wake juu ya kichwa cha hiyo sadaka ya kuteketezwa; nayo itakubaliwa kwa ajili yake, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake. 5 Naye atamchinja huyo ng'ombe mbele ya Bwana; kisha wana wa Haruni, hao makuhani, wataileta karibu hiyo damu, na kuinyunyiza damu yake kando-kando katika madhabahu iliyo hapo mlangoni pa hema ya kukutania 6 Kisha atachuna sadaka ya kuteketeza na kuikata vipande vyake. 7 Kisha wana wa Haruni, watatia moto juu ya madhabahu, na kuzipanga kuni juu ya moto, 8 kisha wana wa Haruni, makuhani, watazipanga kuni zilizo juu ya moto uliopo juu ya madhabahu; 9 lakini matumbo yake, na miguu yake, ataiosha kwa maji; na huyo kuhani ataviteketeza vyote juu ya madhabahu, ili iwe sadaka ya kuteketezwa, dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana. 10 Na matoleo yake kwamba ni katika kundi, katika kondoo, au katika mbuzi, kuwa sadaka ya kuteketezwa; atatoa mume mkamilifu. 11 Naye atamchinja hapo upande wa madhabahu ulioelekea kaskazini mbele za Bwana; na wana wa Haruni, hao makuhani, watainyunyiza damu yake juu ya madhabahu pande zote. 12 Kisha atamkata vipande vyake, pamoja na kichwa chake, na mafuta yake; kisha atavipanga vile vipande juu ya kuni zilizo juu ya madhabahu; 13 lakini matumbo yake, na miguu yake, ataosha kwa maji; na huyo kuhani atavisongeza vyote na kuviteketeza juu ya madhabahu; ni sadaka ya kuteketezwa, dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana. 14 Na matoleo yake atakayomtolea Bwana kuwa sadaka ya kuteketezwa, kwamba ni katika ndege, ndipo atakapoleta matoleo yake katika hua au katika makinda ya njiwa. 15 Kisha kuhani atamleta karibu na madhabahu, naye atamkongonyoa kichwa, na kumteketeza kwa moto juu ya madhabahu; na damu yake itachuruzishwa kando ya madhabahu; 16 kisha atakiondoa kile kibofu chake, pamoja na taka zake, na kukitupa kando ya madhabahu upande wa mashariki, mahali pa majivu; 17 kisha atampasua na mabawa yake, lakini asimkate vipande viwili; kisha kuhani atamteketeza juu ya madhabahu, juu ya kuni zilizo juu ya moto; ni sadaka ya kuteketezwa, dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana.

Mambo ya Walawi 2

1 Na mtu atakapomtolea Bwana matoleo ya sadaka ya unga, matoleo yake yatakuwa ya unga mwembamba; naye ataumiminia mafuta, na kutia na ubani juu yake; 2 kisha atauleta kwa wana wa Haruni, hao makuhani; naye atatwaa konzi moja katika huo unga mwembamba, na katika mafuta yake, na huo ubani wote; kisha kuhani atauteketeza kuwa ndio ukumbusho wake juu ya madhabahu, ni kafara ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana; 3 na huo uliosalia wa ile sadaka ya unga utakuwa ni wa Haruni na wanawe; ni kitu kitakatifu sana katika sadaka zilizosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 4 Tena, utakapotoa matoleo ya sadaka ya unga uliookwa tanuuni, yatakuwa mikate isiyotiwa chachu, ya unga mwembamba uliokandwa na mafuta, au maandazi yasiyochachwa yaliyopakwa mafuta. 5 Tena matoleo yako kwamba ni sadaka ya unga wa kaangoni, yatakuwa ya unga mwembamba usiotiwa chachu, uliokandwa na mafuta. 6 Utaukata-kata vipande, na kutia mafuta juu yake; ni sadaka ya unga. 7 Tena matoleo yako kwamba ni sadaka ya unga ya chunguni, yataandaliwa kwa unga mwembamba pamoja na mafuta. 8 Nawe utamletea Bwana sadaka ya unga iliyofanywa ya vitu hivyo; nayo italetwa kwa kuhani, naye ndiye atakayeisongeza madhabahuni. 9 Kisha kuhani atatwaa humo huo ukumbusho wa sadaka ya unga, naye atauteketeza juu ya madhabahu; ni kafara ya kusongezwa kwa njia ya moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana. 10 Na hicho kitakachosalia katika sadaka ya unga kitakuwa cha Haruni na wanawe; ni kitu kitakatifu sana katika sadaka zilizosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 11 Sadaka ya unga iwayo yote itakayosongezwa kwa Bwana isitiwe chachu kabisa; kwa kuwa hamtateketeza chachu, wala asali iwayo yote, kuwa ni sadaka ya kusongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 12 Vitu hivyo mtavisongeza kwa Bwana kuwa ni malimbuko; lakini visifike juu ya madhabahu kuwa ni harufu ya kupendeza. 13 Tena, kila toleo la sadaka yako ya unga utalitia chumvi; wala usiiache sadaka yako ya unga kupungukiwa na chumvi ya agano la Mungu wako; utatoa chumvi pamoja na matoleo yako yote. 14 Nawe kwamba wamtolea Bwana sadaka ya unga ya malimbuko, utatoa hiyo ngano katika masuke yake iliyochomwa motoni, ngano iliyopondwa ya masuke mabichi, ndiyo utakayoleta kuwa sadaka ya unga ya malimbuko yako. 15 Nawe utatia mafuta juu yake, na kuweka ubani juu yake; ni sadaka ya unga. 16 Huyo kuhani atauteketeza ukumbusho wake, yaani, sehemu ya ngano iliyopondwa ya hiyo sadaka, na sehemu ya mafuta yake, pamoja na ule ubani wake wote; ni kafara ya kusongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto.

Mambo ya Walawi 3

1 Na matoleo yake kwamba ni sadaka za amani; kwamba asongeza katika ng'ombe, mume au mke, atamtoa huyo aliye mkamilifu mbele ya Bwana. 2 Naye ataweka mkono wake kichwani mwake huyo aliyemtoa, na kumchinja mlangoni pa hema ya kukutania; na wana wa Haruni, hao makuhani, watainyunyiza damu yake katika madhabahu pande zote. 3 Naye atasongeza katika sadaka hiyo ya amani, dhabihu kwa Bwana itakayofanywa kwa njia ya moto; yaani, mafuta yafunikayo matumbo, na mafuta yote yaliyo juu ya matumbo, 4 na figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo, yaliyo karibu na kiuno, na hicho kitambi kilicho katika ini, pamoja na hizo figo; hayo yote atayaondoa. 5 Na wana wa Haruni watayateketeza kwa moto juu ya madhabahu, juu ya sadaka ya kuteketezwa, iliyo katika kuni zilizo juu ya moto; ni dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana. 6 Na matoleo yake kwa sadaka za amani atakayomchinjia Bwana, kwamba ni katika kundi la kondoo; mume au mke, atamtoa huyo aliye mkamilifu. 7 Kama akimtoa mwana-kondoo kuwa matoleo yake, ndipo atakapomtolea Bwana; 8 naye ataweka mkono wake kichwani mwake huyo aliyemsongeza, na kumchinja mlangoni pa hema ya kukutania; na wana wa Haruni watainyunyiza damu yake katika madhabahu pande zote. 9 Naye atasongeza katika sadaka hiyo ya amani dhabihu kwa Bwana, itakayofanywa kwa njia ya moto; yaani, mafuta yake, na mkia wenye mafuta mzima, atauondoa kwa kuukata hapo karibu na mfupa wa maungoni; na mafuta yafunikayo matumbo, na mafuta yote yaliyo katika matumbo, 10 na figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo, yaliyo karibu na kiuno chake, na kitambi kilicho katika ini, pamoja na hizo figo; hayo yote atayaondoa. 11 Naye kuhani atayateketeza kwa moto juu ya madhabahu; ni chakula cha dhabihu ya kusongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 12 Na matoleo yake, kwamba ni mbuzi, ndipo atakapomtoa mbele za Bwana; 13 naye ataweka mkono wake kichwani mwake, na kumchinja hapo mbele ya hema ya kukutania; na wana wa Haruni watainyunyiza damu yake katika madhabahu pande zote. 14 Naye atasongeza katika sadaka hiyo matoleo yake, dhabihu kwa Bwana kwa njia ya moto; yaani, mafuta yafunikayo matumbo, na mafuta yote yaliyo katika matumbo, 15 na figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo, yaliyo karibu na kiuno chake, na kitambi kilicho katika ini pamoja na hizo figo mbili; hayo yote atayaondoa. 16 Naye kuhani atayateketeza kwa moto juu ya madhabahu; ni chakula cha dhabihu ya kusongezwa kwa njia ya moto, iwe harufu ya kupendeza; mafuta yote ni ya Bwana. 17 Neno hili litakuwa amri ya daima, katika vizazi vyenu vyote, ndani ya nyumba zenu zote, ya kwamba hamtakula mafuta wala damu kabisa.

Mambo ya Walawi 4

1 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Haya, nena na wana wa Israeli, uwaambie, Kama mtu ye yote akifanya dhambi pasipo kukusudia, katika neno lo lote ambalo Bwana amelizuilia lisifanywe, na kutenda neno lo lote la maneno hayo; 3 kama kuhani aliyetiwa mafuta akifanya dhambi, hata analeta hatia juu ya watu; ndipo na atoe kwa ajili ya dhambi yake aliyoifanya, na kumsongeza kwa Bwana ng'ombe mume mchanga mkamilifu, kuwa ni sadaka ya dhambi. 4 Naye atamleta huyo ng'ombe na kumweka mlangoni pa hiyo hema ya kukutania, mbele za Bwana; naye ataweka mkono wake kichwani mwake ng'ombe, na kumchinja huyo ng'ombe mbele za Bwana. 5 Kisha huyo kuhani aliyetiwa mafuta atatwaa baadhi ya damu ya huyo ng'ombe, na kuileta ndani ya hiyo hema ya kukutania; 6 kisha kuhani atatia kidole chake katika hiyo damu na kuinyunyiza damu mbele ya Bwana mara saba, mbele ya pazia la mahali patakatifu. 7 Kisha kuhani atatia baadhi ya hiyo damu juu ya pembe za madhabahu ya kufukizia uvumba mzuri mbele ya Bwana iliyo ndani ya hema ya kukutania; kisha damu yote ya huyo ng'ombe ataimwaga hapo chini ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, iliyoko mlangoni pa hema ya kukutania. 8 Kisha mafuta yote ya huyo ng'ombe wa sadaka ya dhambi atayaondoa; mafuta yote yafunikayo matumbo, na mafuta yote yaliyo katika matumbo, 9 na figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo, yaliyo karibu na kiuno chake, na kitambi kilicho katika ini, pamoja na hizo figo, hayo yote atayaondoa, 10 vile vile kama yanavyoondolewa katika ng'ombe wa kuchinjwa kwa sadaka za amani; kisha huyo kuhani atayateketeza juu ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa. 11 Kisha ngozi yake ng'ombe, na nyama yake yote, pamoja na kichwa chake, na pamoja na miguu yake, na matumbo yake, na mavi yake, 12 maana, huyo ng'ombe mzima atamchukua nje ya marago hata mahali safi, hapo wamwagapo majivu, naye atamchoma moto juu ya kuni; atachomwa moto hapo majivu yamwagwapo. 13 Na kama mkutano mzima wa Israeli ukifanya dhambi, na jambo lenyewe likayafichamania macho ya huo mkutano, nao wamefanya mojawapo katika mambo yaliyozuiliwa na Bwana, kwamba wasiyafanye, nao wamepata hatia; 14 hapo itakapojulikana hiyo dhambi waliyoifanya, ndipo mkutano utatoa ng'ombe mume mchanga awe sadaka ya dhambi, na kumleta mbele ya hema ya kukutania. 15 Kisha wazee wa mkutano wataweka mikono yao kichwani mwake huyo ng'ombe mbele za Bwana; 16 kisha ng'ombe atachinjwa mbele za Bwana. Kisha kuhani aliyetiwa mafuta atatwaa katika damu ya huyo ng'ombe na kuileta ndani ya hema ya kukutania; 17 kisha kuhani atatia kidole chake katika hiyo damu, na kuinyunyiza mbele za Bwana, mbele ya pazia mara saba. 18 Kisha nyingine katika hiyo damu ataitia katika pembe za madhabahu iliyo mbele za Bwana, iliyoko ndani ya hema ya kukutania, kisha damu yote ataimwaga hapo chini ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, iliyo mlangoni pa hema ya kukutania. 19 Kisha atayaondoa mafuta yake yote na kuyateketeza juu ya madhabahu. 20 Ndivyo atakavyomfanyia huyo ng'ombe; kama alivyomfanyia huyo ng'ombe wa sadaka ya dhambi, atamfanyia na huyu vivyo; naye kuhani atawafanyia upatanisho, nao watasamehewa. 21 Kisha atamchukua huyo ng'ombe nje ya marago, na kumchoma moto vile vile kama alivyomchoma moto ng'ombe wa kwanza; ni sadaka ya dhambi kwa ajili ya mkutano. 22 Mtawala atakapofanya dhambi, na kutenda pasipo kukusudia neno lo lote katika hayo ambayo Bwana, Mungu wake, aliyazuilia yasifanywe, naye amepata hatia; 23 akijulishwa hiyo dhambi yake aliyoifanya, ataleta mbuzi awe matoleo yake, mume, mkamilifu; 24 kisha ataweka mkono wake kichwani mwake huyo mbuzi, na kumchinja hapo wachinjapo sadaka ya kuteketezwa mbele za Bwana; ni sadaka ya dhambi. 25 Kisha kuhani atatwaa katika damu ya hiyo sadaka ya dhambi kwa kidole chake, na kuitia katika pembe za madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, nayo damu yake ataimwaga hapo chini ya madhabahu ya kuteketeza. 26 Na mafuta yake yote atayateketeza juu ya madhabahu, kama alivyoyateketeza mafuta ya hizo sadaka za amani; naye kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya dhambi yake, naye atasamehewa. 27 Na mtu awaye yote katika watu wa nchi akifanya dhambi pasipo kukusudia, kwa kufanya neno lo lote katika hayo ambayo Bwana alizuilia yasifanywe, naye akapata hatia; 28 akijulishwa hiyo dhambi yake aliyoifanya, ndipo atakapoleta mbuzi mke mkamilifu, awe matoleo yake kwa ajili ya dhambi yake aliyoifanya. 29 Naye ataweka mkono wake kichwani mwake hiyo sadaka ya dhambi, na kumchinja sadaka ya dhambi mahali hapo pa sadaka ya kuteketezwa. 30 Kisha kuhani atatwaa katika hiyo damu yake kwa kidole chake, na kuitia katika pembe za madhabahu ya kuteketeza na damu yake yote ataimwaga chini ya madhabahu. 31 Kisha atayaondoa mafuta yake yote, kama vile mafuta yanavyoondolewa katika hizo sadaka za amani; kisha kuhani atayateketeza juu ya madhabahu, iwe harufu ya kupendeza kwa Bwana; na kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake, naye atasamehewa. 32 Naye akileta mwana-kondoo kuwa sadaka ya dhambi, ataleta wa kike mkamilifu. 33 Naye ataweka mkono wake kichwani mwake sadaka ya dhambi, kisha atamchinja awe sadaka ya dhambi, mahali hapo wachinjapo sadaka ya kuteketezwa. 34 Kisha kuhani atatwaa katika hiyo damu ya sadaka ya kuteketezwa kwa kidole chake na kuitia katika pembe za madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, kisha damu yake yote ataimwaga hapo chini ya madhabahu; 35 kisha atayaondoa mafuta yake yote, kama mafuta ya mwana-kondoo yalivyoondolewa katika hizo sadaka za amani; kisha kuhani atayateketeza juu ya madhabahu, kwa desturi ya hizo sadaka za Bwana zilizosongezwa kwa njia ya moto; na kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya hiyo dhambi yake aliyoifanya, naye atasamehewa.

Mambo ya Walawi 5

1 Na mtu awaye yote akifanya dhambi, kwa kuwa ameisikia sauti yenye kuapisha, naye akawa ni shahidi, kwamba aliona au kujua, asipolifunua neno lile, ndipo atakapochukua uovu wake mwenyewe; 2 au kama mtu akigusa kitu kilicho najisi, kama ni mzoga wa mnyama wa nyikani aliye najisi, au kama ni mzoga wa mnyama wa mfugo aliye najisi, au kama ni mzoga wa mdudu aliye najisi, naye jambo hilo linamfichamania, akapata kuwa najisi, ndipo atakapochukua uovu wake; 3 au kama akiugusa uchafu wa binadamu, uchafu uwao wote ambao kwa huo amepata unajisi, na jambo hilo linamfichamania, hapo apatapo kulijua, ndipo atakapokuwa na hatia; 4 au, kama mtu akijiapisha, kwa kutamka haraka kwa midomo yake, kutenda uovu, au kutenda mema, neno lo lote mtu atakalolitamka kwa kiapo pasipo kufikiri, na neno hilo likamfichamania; hapo atakapolijua, ndipo atakapokuwa na hatia katika mambo hayo mojawapo; 5 kisha itakuwa, hapo atakapokuwa na hatia katika mambo hayo mojawapo, ndipo atakapoliungama jambo hilo alilolikosa; 6 naye atamletea Bwana sadaka yake ya hatia kwa ajili ya hiyo dhambi yake aliyoifanya, mwana-kondoo wa kike, au mbuzi mke, kutoka katika kundi lake, kuwa ni sadaka ya dhambi; kisha kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya hiyo dhambi yake. 7 Lakini asipomweza mwana-kondoo, ndipo atakapomletea Bwana hua wawili, au makinda mawili ya njiwa, kuwa ni sadaka yake ya hatia ya jambo hilo alilolikosa; mmoja wa hao ndege kwa sadaka ya dhambi, na wa pili kwa sadaka ya kuteketezwa. 8 Naye atawaleta kwa kuhani, atakayemsongeza kwanza yule wa sadaka ya dhambi, naye atamkongonyoa kichwa shingoni mwake, lakini asimpasue vipande viwili; 9 kisha baadhi ya damu ya hiyo sadaka ya dhambi atainyunyiza katika ubavu wa madhabahu; na damu iliyosalia itachuruzishwa hapo chini ya madhabahu; ni sadaka ya dhambi. 10 Kisha huyo ndege wa pili atamsongeza kuwa sadaka ya kuteketezwa, sawasawa na sheria; na kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya hiyo dhambi yake aliyoifanya, naye atasamehewa. 11 Lakini asipowaweza hua wawili, au makinda mawili ya njiwa, ndipo hapo atakapoleta matoleo yake kwa ajili ya neno hilo alilolikosa, sehemu ya kumi ya efa ya unga mwembamba, kuwa sadaka yake ya dhambi; asitie mafuta juu yake, wala ubani usitiwe juu yake; maana, ni sadaka ya dhambi. 12 Naye atamletea kuhani, na kuhani atatwaa konzi yake ya huo unga kuwa ukumbusho wake, na kuuteketeza juu ya madhabahu, juu ya sadaka zilizosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto; ni sadaka ya dhambi. 13 Na huyo kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya dhambi yake ambayo katika mambo hayo mojawapo amefanya dhambi, naye atasamehewa; na unga uliosalia utakuwa wa kuhani, kama hiyo sadaka ya unga ilivyokuwa. 14 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 15 Mtu awaye yote akiasi na kufanya dhambi naye hakukusudia, katika mambo matakatifu ya Bwana; ndipo atakapomletea Bwana sadaka yake ya hatia, kondoo mume mkamilifu katika kundi lake; sawasawa na hesabu utakayomwandikia katika shekeli za fedha, kwa shekeli ya mahali patakatifu, kuwa sadaka ya hatia; 16 naye atalipa kwa ajili ya hilo alilolikosa katika kitu kile kitakatifu, kisha ataongeza na sehemu ya tano, na kumpa kuhani; naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake kwa huyo kondoo mume wa sadaka ya hatia, naye atasamehewa. 17 Na kama mtu akifanya dhambi, na kutenda mambo hayo mojawapo ambayo Bwana alizuilia yasifanywe, ajapokuwa hakuyajua, ni mwenye hatia vivyo, naye atachukua uovu wake. 18 Naye ataleta kondoo mume wa kundi lake, mkamilifu, sawasawa na hesabu utakayomwandikia, kuwa sadaka ya hatia, amsongeze kwa huyo kuhani; na kuhani atamfanyia upatanisho kwa ajili ya jambo hilo alilolikosa pasipo kukusudia, asilijue, naye atasamehewa. 19 Ni sadaka ya hatia; hakika yake ni mwenye hatia mbele za Bwana.

Mambo ya Walawi 6

1 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Mtu awaye yote akifanya dhambi, na kuasi juu ya Bwana, akamdanganya mwenziwe katika jambo la amana, au la mapatano, au la kunyang'anya, au kumwonea mwenziwe; 3 au kuzumbua kitu kilichopotea na kutenda la uongo juu yake, na kuapa kwa uongo; katika mambo hayo yote mojawapo atakalolitenda mtu, na kufanya dhambi kwalo; 4 ndipo itakapokuwa, akiwa amefanya dhambi, na kupata hatia, atarudisha hicho alichokipata kwa kunyang'anya, au kitu kile alichokipata kwa kuonea, au ile amana aliyowekewa, au kitu kile kilichopotea alichokizumbua yeye, 5 au kitu cho chote ambacho amekiapia uongo; atakirudisha hata kwa utimilifu wake, kisha ataongeza na sehemu ya tano zaidi juu yake; naye atampa huyo mwenyewe, siku hiyo ambayo atakapohukumiwa kuwa mwenye hatia. 6 Kisha ataleta sadaka yake ya hatia kwa Bwana, ni kondoo mume wa katika kundi lake, mkamilifu, sawasawa na hesabu utakayomwandikia, kuwa sadaka ya hatia, na kumpa kuhani; 7 na huyo kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake mbele za Bwana, naye atasamehewa; katika jambo lo lote alifanyalo hata akapata kuwa mwenye hatia kwalo. 8 Bwana akanena na Musa na kumwambia, 9 Haya, mwagize Haruni na wanawe, uwaambie, Amri ya sadaka ya kuteketezwa ni hii; hiyo sadaka ya kuteketezwa itakuwa pale motoni juu ya madhabahu usiku wote hata asubuhi; na huo moto wa madhabahu utawaka juu yake usizimike. 10 Naye kuhani atavaa nguo yake ya kitani, na suruali zake za kitani atazivaa mwilini mwake; naye atayazoa majivu ambayo huo moto umeiteketezea sadaka juu ya madhabahu, kisha atayaweka kando ya madhabahu. 11 Kisha atayavua mavazi yake, na kuvaa mavazi mengine, kisha atayachukua yale majivu kwenda nayo nje ya marago hata mahali safi. 12 Na huo moto ulio madhabahuni atautunza uwake daima juu yake, usizimike; naye kuhani atateketeza kuni katika moto huo kila siku asubuhi; naye ataipanga sadaka ya kuteketezwa juu yake, naye atayateketeza mafuta ya sadaka za amani juu yake. 13 Moto utatunzwa uwake juu ya madhabahu daima; usizimike. 14 Na amri ya hiyo sadaka ya unga ni hii; wana wa Haruni wataisongeza mbele za Bwana, mbele ya madhabahu. 15 Naye atatwaa konzi yake katika huo unga, katika huo unga mwembamba wa sadaka ya unga, na katika mafuta yake, na ubani wote ulio juu ya sadaka ya unga, kisha atauteketeza juu ya madhabahu kuwa harufu ya kupendeza, kuwa ukumbusho wake kwa Bwana. 16 Na unga uliosalia Haruni na wanawe wataula; utaliwa pasipo kutiwa chachu, katika mahali patakatifu; katika ua wa hema ya kukutania ndipo watakapoula. 17 Hautaokwa na chachu. Nimewapa kuwa sehemu yao katika matoleo yangu yasongezwayo kwa njia ya moto; ni kitu kitakatifu sana, kama hiyo sadaka ya dhambi, na kama hiyo sadaka ya hatia. 18 Kila mwana mume miongoni mwa wana wa Haruni atakula katika huo, kuwa ni haki yao milele katika vizazi vyenu, katika matoleo ya Bwana yasongezwayo kwa njia ya moto; mtu awaye yote atakayevigusa atakuwa ni mtakatifu 19 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 20 Matoleo ya Haruni na wanawe watakayomtolea Bwana, katika siku atakayotiwa mafuta, ni haya; sehemu ya kumi ya efa ya unga mwembamba kuwa sadaka ya unga daima, nusu yake asubuhi, na nusu yake jioni. 21 Utaandaliwa kaangoni pamoja na mafuta; ukisha kulowama utauleta ndani; utasongeza hiyo sadaka ya unga vipande vilivyookwa, iwe harufu ya kupendeza kwa Bwana. 22 Na huyo kuhani aliyetiwa mafuta badala yake katika hao wanawe ataisongeza; itateketezwa kabisa kwa Bwana kwa amri ya milele. 23 Tena kila sadaka ya unga ya kuhani itateketezwa kabisa; isiliwe. 24 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 25 Nena na Haruni na wanawe, uwaambie, Amri ya hiyo sadaka ya dhambi ni hii; mahali hapo pachinjwapo sadaka ya kuteketezwa ndipo itakapochinjwa sadaka ya dhambi, mbele za Bwana; ni takatifu sana. 26 Huyo kuhani atakayeisongeza kwa ajili ya dhambi ndiye atakayeila; italiwa katika mahali patakatifu, katika ua wa hema ya kukutania. 27 Kila kitu kitakachoigusa nyama ya sadaka hiyo kitakuwa kitakatifu; tena itakapomwagika damu yake yo yote katika nguo yo yote, utaifua nguo hiyo iliyomwagiwa, katika mahali patakatifu. 28 Lakini hicho chombo cha udongo ambacho hiyo nyama ilipikwa ndani yake kitavunjwa; na kama ikipikwa katika chombo cha shaba, kitasuguliwa, na kuoshwa kwa maji. 29 Kila mwana mume miongoni mwa makuhani atakula katika hiyo; ni takatifu sana. 30 Wala haitaliwa sadaka ya dhambi yo yote, ambayo damu yake yo yote ililetwa ndani ya hema ya kukutania, ili kufanya upatanisho katika mahali patakatifu; itachomwa moto.

Mambo ya Walawi 7

1 Na sheria ya hiyo sadaka ya hatia ni hii; ni takatifu sana. 2 Wataichinja sadaka ya hatia pale pale waichinjapo sadaka ya kuteketezwa; na damu yake atainyunyiza katika madhabahu pande zote. 3 Katika sadaka hiyo atasongeza mafuta yake yote; yaani, mkia wake wenye mafuta, na mafuta yafunikayo matumbo, 4 na figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo, yaliyo karibu na kiuno chake, na kitambi kilicho katika ini, pamoja na figo zake mbili, hayo yote atayaondoa; 5 na kuhani atayateketeza juu ya madhabahu, kuwa dhabihu kwa Bwana kwa njia ya moto; ni sadaka ya hatia. 6 Kila mtu mume miongoni mwa makuhani atakula katika sadaka hiyo; italiwa katika mahali patakatifu; ni takatifu sana. 7 Kama hiyo sadaka ya dhambi ilivyo, na sadaka ya hatia ni vivyo; sheria yake ni moja; huyo kuhani afanyaye upatanisho kwayo, ndiye atakayekuwa nayo. 8 Tena kuhani atakayesongeza sadaka ya kuteketezwa ya mtu awaye yote, huyo kuhani atatwaa awe nayo ngozi ya huyo mnyama wa sadaka ya kuteketezwa aliyemsongeza. 9 Na kila sadaka ya unga iliyookwa mekoni, na yote yaliyoandaliwa chunguni, au kaangoni, yote yatakuwa ya huyo kuhani aliyeyasongeza. 10 Na kila sadaka ya unga, kama umeandaliwa na mafuta, au kama ni mkavu, watautwaa wana wote wa Haruni kuutumia, kila mtu sawasawa. 11 Na sheria ya matoleo ya sadaka za amani, atakazosongeza mtu kwa Bwana, ni hii. 12 Kwamba aitoa kwa ajili ya shukrani, ndipo atakaposongeza pamoja na hiyo sadaka ya shukrani mikate isiyotiwa chachu, iliyoandaliwa na mafuta, na mikate ya kaki isiyochachwa iliyopakwa mafuta, na mikate ya unga mwembamba uliolowama mafuta. 13 Ataleta matoleo yake, pamoja na mikate iliyotiwa chachu, na pamoja na sadaka zake za amani, kwa ajili ya shukrani. 14 Na katika hayo atasongeza kimoja katika kila toleo kiwe sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana; itakuwa ni ya kuhani atakayeinyunyiza hiyo damu ya sadaka za amani. 15 Na hiyo nyama ya sadaka zake za amani zilizochinjwa kwa ajili ya shukrani italiwa siku iyo hiyo ya matoleo yake; asisaze yo yote hata asubuhi. 16 Lakini kwamba hii sadaka ya matoleo yake ni nadhiri, au sadaka ya hiari, italiwa siku hiyo aliyoileta sadaka yake; kisha siku ya pili yake kitakachosalia kitaliwa; 17 lakini hicho kitakachosalia, katika hizo nyama za sadaka, hata siku ya tatu kitachomwa moto. 18 Tena kama nyama yo yote katika hiyo dhabihu yake ya sadaka za amani ikiliwa siku ya tatu, haitakubaliwa, wala haitahesabiwa kwake huyo mwenye kuisongeza; itakuwa ni machukizo, na mtu atakayeila atachukua uovu wake. 19 Tena nyama itakayogusa kitu kilicho najisi haitaliwa; itachomwa moto. Na katika hiyo nyama nyingine, kila mtu aliye safi ana ruhusa kuila; 20 lakini mtu huyo atakayekula katika nyama ya sadaka za amani, ambazo ni za Bwana, na unajisi wake akiwa nao juu yake, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake. 21 Kisha mtu awaye yote atakapogusa kitu cho chote kilicho najisi, uchafu wa binadamu, au mnyama aliye najisi, au machukizo yo yote yaliyo najisi, kisha akala nyama ya dhabihu ya sadaka za amani, ambazo ni za Bwana, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake. 22 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 23 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Msile mafuta yo yote, ya ng'ombe, wala ya kondoo, wala ya mbuzi. 24 Tena mafuta ya mnyama afaye mwenyewe, na mafuta ya mnyama aliyeraruliwa na wanyama, mna ruhusa kuyatumia kwa ajili ya matumizi mengine; lakini msiyale kabisa. 25 Kwani huyo mtu atakayekula mafuta ya mnyama, ambaye ni katika wanyama ambao watu husongeza sadaka kwa Bwana kwa moto, mtu huyo atakayekula mafuta hayo atakatiliwa mbali na watu wake. 26 Tena msiile damu yo yote, ama ya ndege, ama ya mnyama, katika nyumba zenu zote. 27 Mtu ye yote alaye damu, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake. 28 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 29 Nena na wana wa Israeli uwaambie, Yeye asongezaye dhabihu yake ya sadaka za amani kwa Bwana, atamletea Bwana matoleo yake, kutoka katika ile dhabihu ya sadaka zake za amani; 30 mikono yake mwenyewe itamletea hizo sadaka za kusongezwa kwa moto; mafuta yake pamoja na kidari atayaleta, ili kwamba hicho kidari kitikiswe kuwa sadaka ya kutikiswa mbele ya Bwana. 31 Kuhani atayateketeza hayo mafuta juu ya madhabahu; lakini hicho kidari kitakuwa cha Haruni na cha wanawe. 32 Mguu wa nyuma wa upande wa kuume mtampa kuhani kuwa sadaka ya kuinuliwa kutoka katika hizo sadaka zenu za amani. 33 Katika wana wa Haruni, huyo atakayeisongeza damu ya sadaka za amani, na mafuta yake, yeye atapata mguu wa nyuma wa upande wa kuume kuwa sehemu yake. 34 Kwa maana, hicho kidari cha kutikiswa, na huo mguu wa kuinuliwa, nimevitwaa kwa wana wa Israeli, katika dhabihu zao za sadaka za amani, nami nimempa Haruni kuhani na wanawe, kuwa haki yao ya milele kutoka kwa wana wa Israeli. 35 Hii ndiyo sehemu ya Haruni, na sehemu ya wanawe, katika kutiwa mafuta kwao, katika hizo dhabihu zisongezwazo kwa Bwana kwa njia ya moto, siku hiyo aliyowaweka ili wamtumikie Bwana katika kazi ya ukuhani; 36 sehemu ambayo Bwana aliagiza wapewe na wana wa Israeli, siku hiyo aliyowatia mafuta. Ni haki yao ya milele katika vizazi vyao vyote. 37 Sheria ya sadaka ya kuteketezwa ni hii, na ya sadaka ya unga, na ya sadaka ya dhambi, na ya sadaka ya hatia, na ya kuwekwa wakfu, na ya sadaka za amani; 38 ambazo Bwana alimwagiza Musa katika mlima wa Sinai, siku hiyo aliyowaagiza wana wa Israeli wamtolee Bwana matoleo yao, huko katika jangwa la Sinai.

Mambo ya Walawi 8

1 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Mtwae Haruni, na wanawe pamoja naye, na yale mavazi, na mafuta ya kutia, na ng'ombe mume wa sadaka ya dhambi, na kondoo waume wawili, na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu; 3 kisha ukutanishe mkutano wote hapo mlangoni pa hema ya kukutania. 4 Basi Musa akafanya kama alivyoambiwa na Bwana; na huo mkutano ulikutanishwa mlangoni pa hema ya kukutania. 5 Musa akawaambia mkutano, Neno aliloliagiza Bwana kwamba lifanywe, ni hili. 6 Basi Musa akawaleta Haruni na wanawe, akawaosha kwa maji. 7 Kisha akamvika Haruni ile kanzu, na kumfunga mshipi, na kumvika joho, na kumvika naivera, na kumfunga huo mshipi wa kazi ya mstadi wa naivera na kumfunga naivera kwa huo mshipi. 8 Kisha akamtia kile kifuko cha kifuani; akatia hizo Urimu na Thumimu katika hicho kifuko cha kifuani. 9 Akamvika na kile kilemba kichwani mwake; na juu ya kilemba, upande wa mbele, akakitia kile kipande cha dhahabu, hiyo taji takatifu; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 10 Kisha Musa akatwaa hayo mafuta matakatifu ya kutia, akatia mafuta maskani, na vyote vilivyokuwamo, na kuvitakasa. 11 Kisha akanyunyiza hayo mafuta juu ya madhabahu mara saba, na kuitia mafuta madhabahu na vyombo vyake vyote, na birika na tako lake, ili kuvitakasa. 12 Kisha akamimina mafuta hayo ya kutia kichwani mwake Haruni, na kumtia mafuta, ili amtakase. 13 Kisha Musa akawaleta wana wa Haruni, na kuwavika kanzu, na kuwafunga mishipi, na kuwavika vilemba; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 14 Kisha akamleta yule ng'ombe mume wa sadaka ya dhambi; na Haruni na wanawe wakaweka mikono yao katika kichwa cha huyo ng'ombe wa sadaka ya dhambi. 15 Kisha akamchinja; na Musa akaitwaa damu yake, akaitia katika pembe za madhabahu pande zote kwa kidole chake, akaitakasa madhabahu, kisha akaimwaga hiyo damu hapo chini ya madhabahu, na kuitakasa, ili afanye upatanisho kwa ajili yake. 16 Kisha akayatwaa mafuta yote yaliyokuwa katika matumbo yake, na kitambi kilichokuwa katika ini, na figo zake mbili, na mafuta yake, na Musa akayateketeza juu ya madhabahu. 17 Lakini huyo ng'ombe mwenyewe, na ngozi yake, na nyama yake, na mavi yake, akayachoma moto nje ya marago; vile vile kama Bwana alivyomwagiza Musa. 18 Kisha akamsongeza yule kondoo mume wa sadaka ya kuteketezwa; na Haruni na wanawe wakaweka mikono yao kichwani mwa huyo kondoo. 19 Kisha akamchinja; na Musa akainyunyiza damu yake katika madhabahu pande zote. 20 Kisha akamkata kondoo vipande vyake; na Musa akateketeza kichwa, na vile vipande, na mafuta. 21 Kisha akayaosha matumbo na miguu yake kwa maji; na Musa akamteketeza huyo kondoo wote juu ya madhabahu; ilikuwa ni sadaka ya kuteketezwa kuwa harufu ya kupendeza; ilikuwa ni sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 22 Kisha akamsongeza kondoo mume wa pili, huyo kondoo wa kuwaweka wakfu; na Haruni na wanawe wakaweka mikono yao kichwani mwa huyo kondoo. 23 Kisha akamchinja; na Musa akatwaa katika damu yake, na kuitia katika ncha ya sikio la kuume la Haruni, na katika chanda chake cha gumba cha mkono wake wa kuume, na katika kidole cha gumba cha guu lake la kuume. 24 Kisha akawaleta wana wa Haruni, na Musa akaitia hiyo damu katika ncha za masikio ya kuume, na katika vyanda vya gumba vya mikono yao ya kuume, na katika vidole vya gumba vya maguu yao ya kuume; kisha Musa akainyunyiza hiyo damu katika madhabahu pande zote. 25 Kisha akayatwaa hayo mafuta, na mkia wenye mafuta, na mafuta yote yaliyokuwa katika matumbo, na kitambi cha ini, na figo mbili, na mafuta yake, na mguu wa nyuma wa upande wa kuume; 26 kisha katika kikapu cha mikate isiyotiwa chachu, kilichokuwa pale mbele za Bwana, akatwaa mkate mmoja usiochachwa, na mkate mmoja ulioandaliwa na mafuta na kaki moja nyembamba, akaiweka juu ya mafuta, na juu ya huo mguu wa nyuma wa upande wa kuume; 27 kisha akaweka vyote katika mikono ya Haruni, na katika mikono ya wanawe, na kuvitikisa huku na huku viwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana. 28 Kisha Musa akavitwaa tena mikononi mwao, na kuviteketeza juu ya madhabahu, juu ya hiyo sadaka ya kuteketezwa vilikuwa vya kuwaweka wakfu, ni harufu nzuri; ilikuwa dhabihu iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto. 29 Kisha Musa akakitwaa kile kidari, akakitikisa huku na huku, kiwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana; ni sehemu ya Musa katika huyo kondoo mume wa kuwaweka wakfu; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 30 Kisha Musa akatwaa baadhi ya mafuta ya kutia, na ya damu iliyokuwa pale juu ya madhabahu, na kumnyunyizia Haruni, katika mavazi yake, na wanawe, katika mavazi yao, pamoja naye; akamtakasa Haruni, na mavazi yake, na wanawe, na mavazi ya wanawe, pamoja naye. 31 Kisha Musa akawaambia huyo Haruni na wanawe, Tokoseni hiyo nyama mlangoni pa hema ya kukutania; mkaile pale pale, na hiyo mikate iliyo katika kile kikapu cha kuwaweka wakfu, kama nilivyoagizwa kusema, Haruni na wanawe wataila. 32 Nacho kitakachosalia katika hiyo nyama na mikate mtakichoma moto. 33 Wala msitoke nje mlangoni pa hema ya kukutania muda wa siku saba, hata siku za kuwekwa wakfu kwenu zitakapotimia; kwa kuwa atawaweka muda wa siku saba. 34 Vile vile kama vilivyotendeka siku ya leo, ni vivyo Bwana alivyoagiza kufanywa, ili kufanya upatanisho kwa ajili yenu. 35 Nanyi mtakaa mlangoni pa hema ya kukutania muda wa siku saba mchana na usiku, na kuulinda ulinzi wa Bwana ili kwamba msife; kwani ndivyo nilivyoagizwa. 36 Basi Haruni na wanawe wakafanya mambo hayo yote Bwana aliyoyaagiza kwa mkono wa Musa.

Mambo ya Walawi 9

1 Basi ilikuwa siku ya nane, Musa akawaita Haruni na wanawe, pamoja na wazee wa Israeli; 2 akamwambia Haruni, Twaa wewe mwana-ng'ombe mume awe sadaka ya dhambi, na kondoo mume wa sadaka ya kuteketezwa, wakamilifu, ukawasongeze mbele ya Bwana. 3 Nawe utawaambia wana wa Israeli, ukisema, Twaeni mbuzi mume awe sadaka ya dhambi; na mwana-ng'ombe, na mwana-kondoo, wote wa mwaka wa kwanza, wakamilifu, kwa sadaka ya kuteketezwa; 4 na ng'ombe mume, na kondoo mume, kwa sadaka za amani, ili kuwachinja mbele za Bwana; na sadaka ya unga uliochanganywa na mafuta; kwa maana, Bwana hivi leo atawatokea. 5 Nao wakayaleta hayo yaliyoagizwa na Musa wakayaweka mbele ya hema ya kukutania; kisha mkutano wote ukakaribia wakasimama mbele za Bwana. 6 Kisha Musa akasema, Neno aliloliagiza Bwana kwamba mlifanye ni hili; na huo utukufu wa Bwana utawatokea. 7 Musa akamwambia Haruni, Ikaribie madhabahu, uitoe sadaka yako ya dhambi, na sadaka yako ya kuteketezwa, ukafanye upatanisho kwa ajili ya nafsi yako, na kwa ajili ya watu; nawe uitoe hiyo dhabihu ya watu, ukafanye upatanisho kwa ajili yao; kama Bwana alivyoagiza. 8 Basi Haruni akakaribia madhabahuni, akamchinja huyo mwana-ng'ombe wa sadaka ya dhambi, aliyekuwa kwa ajili ya nafsi yake. 9 Kisha wana wa Haruni wakamsongezea Haruni ile damu; naye akatia kidole chake katika damu, na kuitia katika pembe za madhabahu, kisha akaimwaga hiyo damu hapo chini ya madhabahu; 10 lakini mafuta, na figo, na kitambi kilichotoka katika ini ya hiyo sadaka ya dhambi, akaviteketeza juu ya madhabahu, kama Bwana alivyomwagiza Musa. 11 Na nyama, na ngozi akazichoma moto nje ya marago. 12 Naye akaichinja sadaka ya kuteketezwa; na wanawe Haruni wakamsongezea ile damu, naye akainyunyiza katika madhabahu pande zote. 13 Nao wakamletea sadaka ya kuteketezwa kipande kwa kipande, na kichwa; naye akaviteketeza juu ya madhabahu. 14 Kisha akaosha matumbo, na miguu na kuiteketeza juu ya hiyo sadaka ya kuteketezwa madhabahuni. 15 Kisha akaisongeza dhabihu ya watu, akamtwaa mbuzi wa sadaka ya dhambi aliyekuwa kwa hao watu, na kumchinja, na kumtoa kwa ajili ya dhambi kama yule wa kwanza. 16 Kisha akaisongeza sadaka ya kuteketezwa, na kuitoa sawasawa na sheria. 17 Kisha akaisongeza sadaka ya unga, na kutwaa konzi humo, na kuiteketeza juu ya madhabahu, pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya asubuhi. 18 Huyo ng'ombe mume naye akamchinja, na huyo kondoo mume pia, dhabihu ya sadaka za amani, zilizokuwa kwa ajili ya watu; na wanawe Haruni wakamsongezea ile damu, naye akainyunyiza katika madhabahu pande zote, 19 na mafuta ya ng'ombe; na ya kondoo, mkia wake wa mafuta, na hayo yafunikayo matumbo, na figo zake, na kitambi cha ini; 20 nao wakayaweka hayo mafuta juu ya vidari, naye akayateketeza mafuta juu ya madhabahu; 21 na vile vidari, na mguu wa nyuma wa upande wa kuume, Haruni akavitikisa huku na huku viwe sadaka ya kutikiswa mbele ya Bwana; kama Musa alivyoagiza. 22 Kisha Haruni akainua mikono yake na kuielekeza kwa hao watu, akawabariki; kisha akashuka akisha isongeza sadaka ya dhambi, na sadaka ya kuteketezwa, na sadaka za amani. 23 Kisha Musa na Haruni wakaingia ndani ya hema ya kukutania, kisha wakatoka nje, na kuwabarikia watu; na huo utukufu wa Bwana ukawatokea watu wote. 24 Kisha moto ukatoka hapo mbele za Bwana, na kuiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na yale mafuta juu ya madhabahu; watu wote walipouona huo moto wakapiga kelele wakainama kifudifudi.

Mambo ya Walawi 10

1 Na Nadabu na Abihu, wana wa Haruni, wakatwaa kila mtu chetezo chake, wakatia moto ndani yake, wakatia na uvumba, nao wakatoa moto wa kigeni mbele ya Bwana, ambao yeye hakuwaagiza. 2 Kisha moto ukatoka hapo mbele za Bwana, nao ukawala, nao wakafa mbele za Bwana. 3 Ndipo Musa akamwambia Haruni, Jambo hili ni hilo Bwana alilolinena, akisema, Nitatakaswa mimi katika hao wanikaribiao, nami nitatukuzwa mbele ya watu hao wote. Haruni akanyamaza kimya. 4 Musa akawaita Mishaeli na Elisafani, wana wa Uzieli mjombaye Haruni, na kuwaambia, Njoni karibu, mwachukue hawa ndugu zenu, mkawaondoe hapa mbele ya maskani, mwende nao nje ya marago. 5 Basi wakaja karibu, na kuwachukua, hali wamevaa nguo zao, wakawachukua nje ya marago; kama Musa alivyosema. 6 Kisha Musa akamwambia Haruni na wanawe Eleazari na Ithamari, Msiache wazi nywele za vichwani mwenu, wala msiyararue mavao yenu; ili kwamba msife, tena asiukasirikie mkutano wote; lakini ndugu zenu, nyumba yote ya Israeli, na waomboleze kwa ajili ya hicho kichomo alichowasha Bwana. 7 Wala hamtatoka nje mlangoni mwa hema ya kukutania, msije mkafa; kwa sababu mafuta ya kutiwa ya Bwana ya juu yenu. Nao wakafanya kama hilo neno la Musa. 8 Kisha Bwana akanena na Haruni, na kumwambia, 9 Usinywe divai wala kileo cho chote, wewe, wala wanao pamoja nawe, hapo mwingiapo ndani ya hema ya kukutania, ili kwamba msife; amri hii itakuwa ni amri ya milele katika vizazi vyenu; 10 kisha, mpate kupambanua kati ya yaliyo matakatifu na hayo yaliyo ya siku zote, na kati ya yaliyo najisi na hayo yaliyo safi; 11 tena mpate kuwafundisha wana wa Israeli amri hizi zote ambazo Bwana amewaambia kwa mkono wa Musa. 12 Kisha Musa akanena na Haruni, na Eleazari, na Ithamari, hao wanawe waliobaki, Twaeni hiyo sadaka ya unga iliyosalia katika kafara za Bwana zilizotolewa kwa moto, mkaile pasipo kutiwa chachu, pale karibu na madhabahu; kwa kuwa ni takatifu sana; 13 nanyi mtaila katika mahali patakatifu, kwa sababu ni haki yako, na haki ya wanao, katika hizo kafara zisongezwazo kwa Bwana kwa moto; kwani ni hivyo nilivyoagizwa. 14 Na kidari cha kutikiswa, na mguu wa kuinuliwa, mtavila katika mahali palipo safi; wewe, na wanao, na binti zako pamoja nawe; kwa maana vimetolewa kuwa ni haki yako, na haki ya wanao, katika zile kafara za sadaka za amani za wana wa Israeli. 15 Mguu wa kuinuliwa, na kidari cha kutikiswa, Watavileta pamoja na dhabihu zisongezwazo kwa njia ya moto, za hayo mafuta ili kuvitikisa viwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana; kisha vitakuwa ni vyako wewe, na vya wanao pamoja nawe, ni haki yenu milele, kama Bwana alivyoagiza. 16 Kisha Musa akamtafuta sana huyo mbuzi wa sadaka ya dhambi, naye, tazama, alikuwa amekwisha kuchomwa moto; naye akawakasirikia hao Eleazari na Ithamari, wana wa Haruni, hao waliobaki, akawaambia, 17 Kwa nini hamkula hiyo sadaka ya dhambi katika mahali patakatifu, kwa kuwa ni takatifu sana, naye amewapa ninyi ili kuuchukua uovu wa mkutano, na kuwafanyia upatanisho mbele za Bwana? 18 Angalieni, hiyo damu yake haikuletwa ndani ya mahali patakatifu; iliwapasa kuila ndani ya mahali patakatifu, kama nilivyowaagiza. 19 Haruni akamwambia Musa, Angalia, hivi leo wamesongeza sadaka yao ya dhambi, na sadaka yao ya kuteketezwa, mbele za Bwana; kisha mambo kama haya yamenipata; tena kama ningalikula hiyo sadaka ya dhambi hivi leo, je! Lingekuwa ni jambo la kupendeza mbele za macho ya Bwana? 20 Naye Musa aliposikia hayo, yakampendeza.

Mambo ya Walawi 11

1 Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 2 Neneni na wana wa Israeli, mkiwaambia, Wanyama hawa ndio wanyama wenye uhai mtakaowala, katika hayawani wote walio juu ya nchi. 3 Kila mnyama mwenye kwato katika miguu yake, mwenye miguu ya kupasuka kati, mwenye kucheua, katika hayawani, hao ndio mtakaowala. 4 Pamoja na hayo, wanyama hawa hamtawala katika wale wenye kucheua, na katika wale walio na kwato; ngamia, kwa sababu yuacheua lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu. 5 Na wibari, kwa sababu yeye hucheua lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu. 6 Na sungura, kwa sababu hucheua, lakini hana kwato, yeye ni najisi kwenu. 7 Na nguruwe, kwa sababu yeye anazo kwato, ni mwenye miguu iliyopasuka kati, lakini hacheui, yeye ni najisi kwenu. 8 Msiile nyama yao, wala msiiguse mizoga yao; hao ni najisi kwenu. 9 Katika hao wote walio ndani ya maji mtakula hawa; kila aliye na mapezi na magamba, ndani ya hayo maji, na ndani ya bahari, na ndani ya mito, mtakula hao. 10 Na hao wote wasio na mapezi na magamba, ndani ya bahari, na ndani ya mito, katika hao waendao majini, na katika wote wenye uhai, waliomo majini, hao ni machukizo kwenu, 11 watakuwa machukizo kwenu; msiile nyama yao, na mizoga yao itakuwa machukizo kwenu. 12 Kila asiye na mapezi wala magamba aliye ndani ya maji ni machukizo kwenu. 13 Kisha katika ndege hawa watakuwa ni machukizo kwenu; hawataliwa, ndio machukizo; tai, na furukombe, na kipungu; 14 na mwewe, na kozi kwa aina zake, 15 na kila kunguru kwa aina zake; 16 na mbuni, na kirukanjia, na dudumizi, na kipanga kwa aina zake; 17 na bundi, na mnandi, na bundi mkubwa; 18 na mumbi, na mwari, na mderi; 19 na korongo, na koikoi kwa aina zake, na hudihudi, na popo. 20 Tena vyote vitambaavyo vyenye mabawa viendavyo kwa miguu minne, hivi ni machukizo kwenu. 21 Pamoja na hayo, hivi vitambaavyo vyenye mabawa viendavyo kwa miguu minne ni halali kula, hao walio na miguu mirefu, ya kurukia juu ya nchi; 22 katika hao mna ruhusa kuwala; nzige kwa aina zake, na nzige kuu kwa aina zake, na panzi kwa aina zake, na parare kwa aina zake. 23 Lakini vyote vitambaavyo vyenye mabawa, vilivyo na miguu minne, ni machukizo kwenu. 24 Nanyi mtakuwa najisi kwa wanyama hao; kila atakayegusa mzoga wao atakuwa ni najisi hata jioni; 25 na mtu awaye yote atakayechukua cho chote cha mizoga yao atafua nguo zake, naye atakuwa najisi hata jioni. 26 Kila mnyama aliyepasuliwa ukwato, naye hana kwato mbili, wala hacheui, huyo ni najisi kwenu; kila agusaye wanyama hao atakuwa ni najisi. 27 Tena kila mnyama aendaye kwa vitanga vyake, katika hao wanyama wote waendao kwa miguu minne, hao ni najisi kwenu; awaye yote atakayegusa mizoga yao, atakuwa ni najisi hata jioni. 28 Na huyo atakayechukua mzoga wa wanyama hao atafua nguo zake, naye atakuwa ni najisi hata jioni; hao ni najisi kwenu 29 Tena katika vitu vile vitambaavyo, vitambaavyo juu ya nchi, hivi ni najisi kwenu; kicheche, na panya, na mjombakaka, kwa aina zake, 30 na guruguru na kenge, na mjusi na goromoe, na lumbwi. 31 Wanyama hao ndio walio najisi kwenu katika hao watambaao; awaye yote atakayewagusa, wakiisha kufa, atakuwa ni najisi hata jioni. 32 Tena kitu cho chote, wanyama hao mmojawapo atakachokiangukia, wakiisha kufa, kitakuwa ni najisi; kwamba ni chombo cha mti, au nguo, au ngozi, au gunia, chombo cho chote kitakachoangukiwa, ambacho ni chombo cha kufanyia kazi yo yote, lazima kitiwe ndani ya maji, nacho kitakuwa ni najisi hata jioni; ndipo kitakapokuwa ni safi. 33 Na kila chombo cha udongo, wanyama hao mmojawapo atakachokiangukia, kila kilichomo ndani yake kitakuwa ni najisi, na hicho chombo kitavunjwa. 34 Kila chakula kilichomo, ambacho ni kuliwa, hicho ambacho maji hutumiwa juu yake, kitakuwa ni najisi; na kila kinyweo ambacho ni cha kunywewa, kilichomo katika chombo kama hicho, kitakuwa ni najisi. 35 Na kila kitu kitakachoangukiwa na kipande cho chote cha mizoga yao kitakuwa najisi; kwamba ni tanuru, au meko ya vyungu, kitavunjwa vipande vipande; ni najisi vitu hivyo, navyo vitakuwa najisi kwenu. 36 Pamoja na hayo, chemchemi, au shimo, ambamo maji yakusanyika, vitakuwa ni safi; lakini hicho kitakachogusa mizoga yao kitakuwa ni najisi. 37 Na kipande cho chote cha mzoga kikiwa kimeangukia mbegu za kupandwa zitakazopandwa, zitakuwa safi. 38 Lakini kwamba hizo mbegu zilitiwa maji na cho chote cha mizoga yao kuziangukia, ni najisi kwenu. 39 Kama akifa mnyama awaye yote, ambaye mna ruhusa kumla, yeye anayeugusa mzoga wake atakuwa najisi hata jioni. 40 Na yeye atakayekula nyama ya mzoga wake atafua nguo zake, naye atakuwa najisi hata jioni; yeye atakayeuchukua mzoga wake atafua nguo zake, naye atakuwa ni najisi hata jioni. 41 Na kila kitu kitambaacho juu ya nchi ni machukizo; hakitaliwa. 42 Kila aendaye kwa tumbo lake, na kila aendaye kwa miguu minne, na kila aendaye kwa miguu mingi, maana, ni vyote vyenye kutambaa vitambaavyo juu ya nchi, hamtavila, kwa kuwa ni machukizo. 43 Msifanye nafsi zenu kuwa ni chukizo kwa kitu cho chote chenye kutambaa, kitambaacho, wala msifanye nafsi zenu kuwa ni najisi kwa vitu hivyo, mkajipatia uchafu kwa hivyo. 44 Kwa kuwa mimi ni Bwana, Mungu wenu; takaseni nafsi zenu basi; iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu; wala msitie uchafu nafsi zenu kwa kitu kitambaacho cha aina yo yote, kiendacho juu ya nchi. 45 Kwa kuwa mimi ni Bwana niliyewaleta kutoka nchi ya Misri, ili kwamba niwe Mungu wenu; basi mtakuwa watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu. 46 Hii ndiyo sheria katika hao wanyama, na ndege, na kila kiumbe kilicho hai, kiendacho ndani ya maji, na kila kiumbe kitambaacho juu ya nchi; 47 ili kupambanua kati ya hao walio najisi na hao walio safi, na kati ya kiumbe kilicho hai ambacho chaliwa, na hicho kilicho hai ambacho hakiliwi.

Mambo ya Walawi 12

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na hao wana wa Israeli, uwaambie, Mwanamke akitunga mimba na kuzaa mtoto mume, ndipo atakuwa yu najisi siku saba; kama katika siku za kutengwa kwake kwa ajili ya hedhi, ndivyo atakavyokuwa najisi. 3 Siku nane mtoto atatahiriwa govi ya zunga lake. 4 Na huyo mwanamke atakaa katika damu ya kutakata kwake siku thelathini na tatu; asiguse kitu kilicho kitakatifu, wala asiingie mahali patakatifu, hata siku hizo za kutakata kwake zitakapotimia. 5 Lakini kwamba amezaa mtoto mke ndipo atakuwa najisi juma mbili, kama katika kutengwa kwake; naye atakaa katika damu ya kutakata kwake muda wa siku sitini na sita. 6 Kisha hizo siku za kutakaswa kwake zitakapotimia, kwa ajili ya mwana, au kwa ajili ya binti, ataleta mwana-kondoo wa mwaka mmoja kuwa sadaka ya kuteketezwa na kinda la njiwa, au hua, kuwa sadaka ya dhambi, awalete mlangoni pa hema ya kukutania, na kumpa kuhani; 7 na yeye atawasongeza mbele za Bwana, na kufanya upatanisho kwa ajili yake; naye atatakasika na jicho la damu yake. Hii ndiyo amri yake huyo azaaye, kwamba ni mtoto mume au mke. 8 Kama mali yake huyo mwanamke haimfikilii mwana-kondoo, hapo ndipo atakapochukua hua wawili, au makinda mawili ya njiwa; mmoja kuwa sadaka ya kuteketezwa, na wa pili kuwa sadaka ya dhambi; naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake, naye atakuwa safi.

Mambo ya Walawi 13

1 Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 2 Mtu atakapokuwa na kivimbe katika ngozi ya mwili wake, au kikoko, au kipaku king'aacho, nalo likawa pigo la ukoma katika ngozi ya mwili wake, ndipo atakapoletwa kwa Haruni kuhani, au kwa wanawe, makuhani mmojawapo; 3 na huyo kuhani ataliangalia hilo pigo lililo katika ngozi ya mwili; na kwamba malaika yaliyo katika hilo pigo yamegeuka kuwa meupe, na hilo pigo kuonekana kwake limeingia ndani kuliko ile ngozi ya mwili wake, ni pigo la ukoma hilo; na kuhani atamwangalia na kusema kuwa yu mwenye unajisi. 4 Na hicho kipaku king'aacho, kwamba ni cheupe katika ngozi ya mwili wake, na kuonekana kwake si shimo la kuingia ndani kuliko ngozi, na malaika hayakugeuka kuwa meupe, ndipo kuhani atamweka mahali muda wa siku saba huyo aliye na hilo pigo; 5 kisha kuhani atamwangalia siku ya saba; naye akiona ya kuwa pigo limeshangaa, na pigo halikwendelea mbele katika ngozi yake, ndipo kuhani atamweka mahali muda wa siku saba tena; 6 kisha siku ya saba kuhani atamwangalia tena; na tazama, ikiwa hilo pigo limeanza kufifia, wala pigo halikwendelea mbele katika ngozi yake, ndipo kuhani atasema kuwa yu safi; ni kikoko; naye atazifua nguo zake, kisha atakuwa yu safi. 7 Lakini kwamba kikoko kimeenea katika ngozi yake baada ya kuonyesha nafsi yake kwa kuhani kwa kupata kutakaswa kwake ataonyesha nafsi yake tena kwa kuhani; 8 na kuhani ataangalia, na tazama ikiwa hicho kikoko kimeenea katika ngozi, ndipo kuhani atasema kuwa yu najisi; ni ukoma. 9 Pigo la ukoma litakapokuwa katika mtu, ndipo ataletwa kwa kuhani; 10 na kuhani ataangalia, na tazama, ikiwa pana kivimbe cheupe katika ngozi yake, na malaika yamegeuzwa kuwa meupe, tena ikiwa pana nyama mbichi iliyomea katika kile kivimbe, 11 ni ukoma wa zamani ulio katika ngozi ya mwili wake, na kuhani atasema kuwa yu najisi; hatamweka mahali, kwa kuwa yeye yuna unajisi. 12 Tena kwamba huo ukoma ukitokeza katika ngozi yake, na ukoma ukamwenea ngozi yote, tangu kichwa hata miguuni, kama aonavyo kuhani; 13 ndipo huyo kuhani ataangalia; na tazama, ikiwa ukoma umemwenea mwili wake wote, atasema kuwa yu safi huyo aliye na hilo pigo umegeuka kuwa mweupe wote; yeye ni safi. 14 Lakini po pote itakapoonekana nyama mbichi kwake mtu huyo, atakuwa yu najisi. 15 Kuhani ataiangalia hiyo nyama mbichi, naye atasema kuwa yu najisi; ile nyama mbichi ni najisi; ni ukoma. 16 Au kama hiyo nyama mbichi iligeuka tena, na kugeuzwa kuwa nyeupe, ndipo atamwendea kuhani, 17 na huyo kuhani atamwangalia; na tazama, ikiwa hilo pigo limegeuzwa kuwa jeupe, ndipo huyo kuhani atasema kuwa yu safi huyo aliyekuwa na pigo; yeye yu safi. 18 Tena mwili wa mtu utakapokuwa na jipu katika ngozi yake, nalo limepoa, 19 na mahali palipokuwa na lile jipu pana kivimbe cheupe, au kipaku king'aacho, cheupe lakini chekundu kidogo, ndipo atamwonyesha kuhani mahali hapo; 20 na kuhani ataangalia, na tazama, kwamba kumeonekana kuingia ndani kuliko ngozi yenyewe, na malaika yakiwa yamegeuka kuwa meupe, ndipo kuhani atasema kwamba yu najisi; ni pigo la ukoma limetokea katika hilo jipu. 21 Lakini kuhani akipaangalia, na tazama hamna malaika meupe ndani yake, wala hapana pa kuingia ndani kuliko ile ngozi, lakini paanza kufifia, ndipo kuhani atamweka mahali muda wa siku saba; 22 na kwamba pameenea katika ngozi, ndipo kuhani atasema kwamba yu najisi; hili ni pigo. 23 Lakini ikiwa kipaku hicho king'aacho kimeshangaa pale pale, wala hakienei, ni kovu ya jipu; na kuhani atasema kwamba yu safi. 24 Au mwili wa mtu ukiwa una mahali katika ngozi yake penye moto, na hiyo nyama iliyomea pale penye moto, kama kikiwa kipaku chekundu kidogo, au cheupe; 25 ndipo kuhani atapaangalia; na tazama, yakiwa malaika yaliyo katika kile kipaku yamegeuka kuwa meupe, na kwamba kumeonekana kuingia ndani kuliko ngozi yenyewe; ni ukoma, umetokea katika mahali penye moto; na kuhani atasema kwamba yu najisi; hili ni pigo la ukoma. 26 Lakini kuhani akipaangalia, na tazama, malaika meupe hamna katika hicho kipaku king'aacho, nacho hakikuingia ndani kuliko ngozi, lakini chafifia; ndipo kuhani atamweka mahali muda wa siku saba; 27 na kuhani atamwangalia siku ya saba; kama kimeenea katika ngozi, ndipo huyo kuhani atasema kwamba yu najisi; hili ni pigo la ukoma. 28 Na kama hicho kipaku kikishangaa pale pale, wala hakikuenea katika ngozi, lakini kimefifia; ni kufura kwake pale penye moto, na kuhani atasema kwamba yu safi; kwa kuwa ni kovu la kuwasha hili. 29 Tena mtu, mume au mke, akiwa na pigo juu ya kichwa, au katika ndevu zake, 30 ndipo kuhani ataliangalia hilo pigo; na tazama, kwamba kumeonekana kuingia ndani kuliko ngozi yenyewe, tena zikiwamo nywele za rangi ya manjano kisha nyembamba, ndipo kuhani atasema kwamba yu najisi, maana, ni kipwepwe, ni ukoma wa kichwa, au wa ndevu. 31 Tena kuhani akiliangalia lile pigo la kipwepwe, na tazama, kwamba kumeonekana si kuingia ndani kuliko ngozi yenyewe, wala hamna nywele nyeusi ndani yake, ndipo kuhani atamweka mahali huyo aliye na pigo la kipwepwe muda wa siku saba; 32 na siku ya saba kuhani ataliangalia hilo pigo; na ikiwa hicho kipwepwe hakikuenea, wala hamna nywele za rangi ya manjano ndani yake, na kwamba kipwepwe hakionekani kuingia ndani kuliko ngozi yenyewe, 33 ndipo huyo mtu atanyolewa, lakini hicho kipwepwe hatakinyoa; na kuhani atamweka mahali huyo aliye na kipwepwe muda wa siku saba tena; 34 na siku ya saba kuhani atakiangalia hicho kipwepwe, na tazama, ikiwa kipwepwe hakikuenea katika ngozi yake, wala hakionekani kuingia ndani kuliko ngozi; ndipo huyo kuhani atasema kwamba yu safi; naye atazifua nguo zake, naye atakuwa yu safi. 35 Lakini hicho kipwepwe kama kikienea katika ngozi yake baada ya kutakasika kwake; 36 ndipo kuhani atamwangalia; na ikiwa hicho kipwepwe kimeenea katika ngozi yake, kuhani hatatafuta hizo nywele za rangi ya manjano; yeye yu najisi. 37 Lakini akiona ya kuwa hicho kipwepwe kimeshangaa, na nywele nyeusi zimemea humo; hicho kipwepwe kimepoa, naye yu safi, na huyo kuhani atasema kwamba yu safi. 38 Mtu, mume au mke, atakapokuwa na vipaku ving'aavyo katika ngozi ya mwili, vipaku ving'aavyo vyeupe; 39 ndipo kuhani ataangalia; na tazama, ikiwa vile vipaku ving'aavyo vilivyo katika ngozi ya mwili wake ni vyeupe kidogo; ni mba hivyo, imetokea katika ngozi; yeye yu safi. 40 Kwamba nywele za mtu zimemtoka kichwani mwake, yeye ni mwenye upaa, yu safi. 41 Tena kwamba nywele za mtu zimemtoka kichwani upande wa mbele, yeye ni mwenye upaa wa kipaji; yu safi. 42 Lakini kwamba katika kile kichwa kilicho na upaa, au kile kipaji kilicho na upaa, laonekana pigo jeupe kisha jekundu kidogo; ni ukoma, unatokea katika kichwa chake cha upaa, au katika kipaji chake cha upaa. 43 Ndipo kuhani atamwangalia; na tazama, kivimbe cha pigo kikiwa cheupe na chekundu-chekundu, katika kichwa chake chenye upaa, au katika kipaji chake cha upaa, kama vile kuonekana kwa ukoma katika ngozi ya mwili; 44 yeye ni mtu mwenye ukoma, yu najisi; na kuhani hana budi atasema kuwa yu najisi; pigo lake li katika kichwa chake. 45 Kisha mwenye ukoma aliye na pigo ndani yake, nguo zake zitararuliwa, na nywele za kichwa chake zitaachwa wazi, naye atafunika mdomo wake wa juu, naye atapiga kelele, Ni najisi, ni najisi. 46 Siku zote ambazo pigo li ndani yake, yeye atakuwa mwenye unajisi; yeye yu najisi; atakaa peke yake; makazi yake yatakuwa nje ya marago. 47 Tena, vazi nalo ambalo pigo la ukoma li ndani yake, kwamba ni vazi la sufu, au kwamba ni la kitani; 48 likiwa limefumwa, au kusokotwa; likiwa ni la kitani au la sufu; kwamba ni katika ngozi, au kitu cho chote kilichofanywa cha ngozi; 49 hilo pigo likiwa la rangi ya majani au jekundu, katika vazi, au katika ngozi, au katika lililofumwa, au katika lililosokotwa, au katika kitu cho chote cha ngozi; ni pigo la ukoma, nalo ataonyeshwa kuhani; 50 na kuhani ataliangalia hilo pigo, naye atakiweka mahali kile kilicho na pigo muda wa siku saba; 51 kisha siku ya saba ataliangalia hilo pigo; kama pigo limeenea katika hilo lililofumwa, au katika hilo lililosokotwa, au katika ngozi, ijapokuwa hiyo ngozi ina matumizi yo yote; hilo pigo ni ukoma unaokula; vazi hilo ni najisi. 52 Naye atalichoma moto vazi hilo, kwamba ni lililofumwa au kwamba ni lililosokotwa, kama ni la sufu, au la kitani, au kitu cho chote cha ngozi, ambacho kina hilo pigo ndani yake; kwa maana, ni ukoma unaokula; vazi hilo litachomwa moto; 53 Na kama kuhani akitazama, na tazama, ikiwa hilo pigo halikuenea katika hilo vazi, wala katika hilo lililofumwa, wala katika hilo lililosokotwa, wala katika kitu cho chote cha ngozi; 54 ndipo kuhani ataamuru kwamba wakifue kitu kile kilicho na hilo pigo, naye atakiweka mahali muda wa siku saba tena; 55 kisha kuhani ataangalia, baada ya kuoshwa hilo pigo; na tazama, ikiwa hilo pigo halikugeuka rangi yake, wala halikuenea, li najisi; utakichoma moto; ni uharibifu likiwa lina upaa ndani au nje. 56 Huyo kuhani akiangalia, na tazama, ikiwa hilo pigo limeanza kufifia, baada ya kufuliwa kwake, ndipo atalirarua hilo pigo litoke katika vazi, au katika ngozi, au katika lililofumwa, au katika lililosokotwa; 57 kisha, likionekana li vivyo katika hilo vazi, katika lililofumwa, au katika lililosokotwa, au katika kitu cho chote cha ngozi, ni pigo lenye kuenea; nawe vazi hilo lenye pigo utalichoma moto. 58 Na hilo vazi, lililofumwa, au lililosokotwa, au kitu cho chote cha ngozi, utakalolifua, kama hilo pigo limetoka na kuliacha, ndipo litafuliwa mara ya pili, nalo litakuwa safi. 59 Na katika pigo la ukoma katika vazi la sufu, au la kitani, kama ni katika lililofumwa, au lililosokotwa, au katika kitu cho chote cha ngozi, sheria yake ni hiyo, kusema kwamba ni safi, au kusema kwamba ni najisi.

Mambo ya Walawi 14

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Hii ndiyo sheria ya mwenye ukoma, katika siku ya kutakaswa kwake; ataletwa kwa kuhani, 3 na huyo kuhani atatoka aende nje ya marago; na kuhani ataangalia, na tazama, ikiwa pigo la ukoma limepoa kwake huyo mwenye ukoma; 4 ndipo huyo kuhani ataagiza kwamba watwae kwa ajili yake atakayetakaswa ndege wawili walio hai, ambao ni safi, na mti wa mwerezi, na sufu nyekundu, na hisopo; 5 kisha kuhani ataagiza ndege mmoja achinjwe katika chombo cha udongo kilicho juu ya maji ya mtoni; 6 kisha huyo ndege aliye hai atamshika, na huo mti wa mwerezi, na hiyo sufu nyekundu, na hisopo, naye atavichovya hivyo, pamoja na yule ndege aliye hai, katika damu ya huyo ndege aliyechinjwa juu ya maji ya mtoni; 7 kisha atamnyunyizia huyo atakayetakaswa na ukoma mara saba, naye atasema kwamba yu safi, kisha atamwacha yule ndege aliye hai aende zake nyikani. 8 Naye huyo atakayetakaswa atazifua nguo zake, na kunyoa nywele zake zote, na kuoga katika maji, naye atakuwa safi; baada ya hayo ataingia ndani ya marago, lakini ataketi nje ya hema yake muda wa siku saba. 9 Kisha siku ya saba atanyoa nywele zote za kichwani mwake, na ndevu zake, na nyushi zake, nywele zake zote pia atazinyoa; kisha atazifua nguo zake, na kuoga mwili wake majini, naye atakuwa safi. 10 Kisha siku ya nane atachukua wana-kondoo wawili waume wakamilifu, na mwana-kondoo mmoja wa kike wa mwaka wa kwanza mkamilifu, na sehemu tatu za kumi za efa moja ya unga mwembamba kuwa sadaka ya unga, kuchanganywa na mafuta, na logi moja ya mafuta. 11 Kisha kuhani atakayemtakasa atamsimamisha huyo mtu atakayetakaswa, pamoja na vitu vile vyote, mbele za Bwana, mlangoni pa hema ya kukutania; 12 kisha kuhani atamshika mmoja katika hao wana-kondoo waume, na kumsongeza awe sadaka ya hatia, pamoja na hiyo logi ya mafuta, kisha atavitikisa kuwa ni sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana; 13 kisha atamchinja huyo mwana-kondoo mahali hapo wachinjapo sadaka ya dhambi na sadaka ya kuteketezwa, ndani ya mahali patakatifu; kwa kuwa kama hiyo sadaka ya dhambi ilivyo ya kuhani, ni vivyo sadaka ya hatia; ni takatifu sana; 14 kisha huyo kuhani atatwaa katika hiyo damu ya sadaka ya hatia, naye kuhani ataitia katika ncha ya sikio la kuume la huyo atakayetakaswa, na katika chanda cha gumba cha mkono wake wa kuume, na katika kidole kikuu cha mguu wake wa kuume; 15 kisha kuhani atatwaa katika hiyo logi ya mafuta, na kuyamimina katika kitanga cha mkono wake mwenyewe wa kushoto; 16 kisha kuhani atatia kidole cha mkono wa kuume katika hayo mafuta, yaliyo katika mkono wake wa kushoto, naye atayanyunyiza hayo mafuta kwa kidole chake mara saba mbele za Bwana; 17 na katika yale mafuta yaliyobaki mkononi mwake kuhani atayatia katika ncha ya sikio la kuume la huyo atakayetakaswa, na katika chanda cha gumba cha mkono wake wa kuume, na katika kidole kikuu cha mguu wake wa kuume, juu ya damu ya sadaka ya hatia; 18 na mafuta yaliyobaki, yaliyo katika mkono wa kuhani, atayatia juu ya kichwa cha huyo atakayetakaswa; na kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake, mbele za Bwana. 19 Kisha kuhani atasongeza sadaka ya dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili yake huyo atakayetakaswa kwa sababu ya unajisi wake; kisha baadaye ataichinja sadaka ya kuteketezwa; 20 kisha kuhani ataisongeza hiyo sadaka ya kuteketezwa, na sadaka ya unga, juu ya madhabahu na kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake, naye atakuwa safi. 21 Tena kwamba ni maskini, naye hawezi kupata kiasi hicho, ndipo atatwaa mwana-kondoo mmoja wa kiume, awe sadaka ya hatia ya kutikiswa, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake, na sehemu ya kumi ya efa ya unga mwembamba, uliochanganywa na mafuta kuwa sadaka ya unga, na logi ya mafuta; 22 na hua wawili, au makinda mawili ya njiwa, kama awezavyo kuwapata; huyo mmoja atakuwa sadaka ya dhambi, na wa pili atakuwa sadaka ya kuteketezwa. 23 Hata siku ya nane atawaleta kwa kuhani, mlangoni pa hema ya kukutania mbele za Bwana, kwa ajili ya kutakaswa kwake. 24 Na kuhani atamtwaa huyo mwana-kondoo wa sadaka ya hatia, na hiyo logi ya mafuta, naye kuhani atavitikisa viwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana; 25 kisha atamchinja mwana-kondoo wa sadaka ya hatia, na kuhani atatwaa katika damu ya sadaka ya hatia, na kuitia katika ncha ya sikio la kuume la huyo atakayetakaswa, na katika chanda cha gumba cha mkono wake wa kuume, na katika kidole kikuu cha mguu wake wa kuume; 26 kisha kuhani atamimina sehemu ya hayo mafuta katika kitanga cha mkono wake mwenyewe wa kushoto; 27 kisha kuhani atanyunyiza baadhi ya hayo mafuta yaliyo katika mkono wake wa kushoto, kwa kidole chake cha mkono wa kuume mara saba mbele za Bwana; 28 kisha kuhani atatia mengine katika hayo mafuta yaliyo mkononi mwake katika ncha ya sikio la kuume la huyo atakayetakaswa, na katika chanda cha gumba cha mkono wake wa kuume, na katika kidole kikuu cha mguu wake wa kuume, juu ya mahali pale penye damu ya sadaka ya hatia; 29 na mafuta yaliyobaki katika mkono wa kuhani atayatia juu ya kichwa cha huyo atakayetakaswa, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake mbele za Bwana. 30 Kisha atasongeza hao hua mmojawapo, au hao makinda ya njiwa mmojawapo, kadiri ya awezao kuwapata; 31 hata kadiri aliyoweza, mmoja kuwa sadaka ya dhambi, na wa pili kuwa sadaka ya kuteketezwa, pamoja na sadaka ya unga; na huyo kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake huyo atakayetakaswa mbele za Bwana. 32 Huyo ambaye ndani yake mna pigo la ukoma, ambaye hawezi kukipata hicho kipasacho kutakaswa kwake, sheria yake ni hiyo. 33 Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 34 Hapo mtakapoingia nchi ya Kanaani, ambayo nawapa kuwa ni milki yenu, nami nitakapolitia pigo la ukoma katika nyumba ya nchi hiyo ya milki yenu; 35 ndipo mwenye nyumba hiyo atakwenda na kumwambia kuhani, akisema, Naona mimi ya kwamba pana kama pigo katika nyumba yangu; 36 ndipo kuhani ataagiza kwamba watoe vyote vilivyomo nyumbani, mbele ya kuhani hajaingia ndani kuliangalia hilo pigo, ili kwamba vyote vilivyomo nyumbani visiwekwe kuwa unajisi; kisha baadaye kuhani ataingia ndani ya nyumba hiyo aitazame; 37 naye ataliangalia hilo pigo, na tazama, likiwa pigo limo ndani ya kuta za nyumba, nalo lina mashimo-mashimo, rangi ya majani, au mekundu, na kuonekana kuingia ndani kuliko huo ukuta; 38 ndipo kuhani atatoka katika nyumba hiyo mpaka mlangoni pa nyumba, na kuifunga hiyo nyumba muda wa siku saba; 39 siku ya saba kuhani atakwenda tena, naye ataangalia; na tazama, likiwa pigo limeenea katika kuta za nyumba; 40 ndipo kuhani atawaambia wayatoe hayo mawe, yaliyo na pigo, na kuyatupa mahali penye uchafu nje ya mji; 41 naye atafanya kwamba hiyo nyumba ikwanguwe ndani pande zote, na chokaa watakayokwangua wataimwaga nje ya mji mahali palipo na uchafu; 42 kisha watatwaa mawe mengine, na kuyatia mahali pa mawe hayo; naye atatwaa chokaa nyingine, na kuipaka chokaa hiyo nyumba. 43 Na kama hilo pigo likirudi tena, na kutokea ndani ya nyumba, baada ya yeye kuyatoa hayo mawe, na baada ya kuikwangua nyumba, na baada ya kupakwa chokaa, 44 ndipo kuhani ataingia ndani na kuangalia, na tazama, likiwa pigo limeenea ndani ya hiyo nyumba, ni ukoma unaokula hiyo nyumba; ni katika unajisi. 45 Naye ataibomoa nyumba, mawe yake, na miti yake, na chokaa yote ya hiyo nyumba; naye atavichukua vyote nje ya mji hata mahali palipo na uchafu. 46 Tena mtu atakayeingia ndani ya hiyo nyumba wakati huo wote iliofungwa, atakuwa najisi hata jioni. 47 Na mtu alalaye ndani ya nyumba hiyo atazifua nguo zake, naye alaye chakula ndani ya nyumba hiyo atazifua nguo zake. 48 Tena kwamba kuhani akiingia ndani na kuangalia, na tazama, ikiwa pigo halikuenea katika hiyo nyumba, baada ya nyumba kupakwa chokaa; ndipo kuhani atasema kwamba hiyo nyumba i safi, maana, pigo limepoa. 49 Naye atatwaa ndege wawili, na mti wa mwerezi, na sufu nyekundu, na hisopo, kwa kuitakasa hiyo nyumba; 50 naye atamchinja mmojawapo wa ndege hao katika chombo cha udongo kilicho juu ya maji ya mtoni; 51 kisha atatwaa huo mti wa mwerezi, na hisopo, na sufu nyekundu, pamoja na huyo ndege aliye hai, na kuvichovya vyote katika damu ya huyo ndege aliyechinjwa, na katika hayo maji ya mtoni, na kuinyunyiza nyumba mara saba; 52 naye ataitakasa hiyo nyumba kwa damu ya ndege, na kwa maji ya mtoni, na kwa huyo ndege aliye hai, na kwa mti wa mwerezi, na kwa hisopo, na kwa sufu nyekundu; 53 lakini ndege aliye hai atamwacha atoke mle mjini aende nyikani; ndivyo atakavyofanya upatanisho kwa ajili ya hiyo nyumba; nayo itakuwa safi. 54 Hiyo ndiyo sheria ya pigo la ukoma ya kila aina, na ya kipwepwe; 55 na ya ukoma wa vazi, na ukoma wa nyumba; 56 na kivimbe, na kikoko na kipaku king'aacho; 57 ili kufunza itakapokuwa ni unajisi, na itakapokuwa ni safi; hiyo ndiyo sheria ya ukoma.

Mambo ya Walawi 15

1 Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 2 Haya, semeni na wana wa Israeli, mkawaambie, Mtu ye yote atakapokuwa na kisonono kimtokacho mwilini mwake, atakuwa najisi kwa ajili ya kisonono chake. 3 Na unajisi wake katika kisonono chake ni huu; kama mwili wake unachuruzika kisonono chake, au kama kisonono chake kimezuiwa mwilini mwake, ni unajisi wake. 4 Kitanda cho chote akilaliacho mwenye kisonono kitakuwa najisi; na kitu cho chote ambacho akiketia kitakuwa najisi. 5 Mtu ye yote atakayekigusa kitanda chake huyo, atazifua nguo zake, na kuoga mwili wake majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 6 Na mtu atakayeketi katika kitu cho chote alichokiketia mwenye kisonono, atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 7 Na mtu atakayegusa mwili wake mwenye kisonono atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 8 Tena kama mwenye kisonono akimtemea mate mtu aliye safi; ndipo atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa yu najisi hata jioni. 9 Na tandiko lo lote atakalolipanda mwenye kisonono litakuwa najisi. 10 Mtu awaye yote atakayegusa kitu cho chote kilichokuwa chini yake huyo atakuwa najisi hata jioni; na mtu atakayevichukua vitu vile atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 11 Na mtu ye yote atakayeguswa na mwenye kisonono, asipokuwa amenawa mikono yake majini, atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 12 Na chombo cha udongo ambacho amekigusa mwenye kisonono, kitavunjwa-vunjwa; na kila chombo cha mti kitaoshwa majini. 13 Na huyo aliye na kisonono atakapotakaswa na kisonono chake, atajihesabia siku saba kwa kutakaswa kwake, naye atazifua nguo zake; naye ataoga mwili wake katika maji ya mtoni, naye atakuwa safi. 14 Na siku ya nane atajipatia hua wawili, au makinda mawili ya njiwa, naye atakwenda mbele za Bwana mlangoni pa hema ya kukutania, naye atampa kuhani hao ndege; 15 na kuhani atawasongeza, mmoja kuwa sadaka ya dhambi, na wa pili kuwa sadaka ya kuteketezwa; naye kuhani atafanya upatanisho mbele za Bwana kwa ajili ya kisonono chake. 16 Na mtu ye yote akitokwa na shahawa yake, ndipo ataoga mwili wake wote majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 17 Na kila nguo, na kila ngozi, ambayo ina shahawa, itafuliwa kwa maji, nayo itakuwa najisi hata jioni. 18 Huyo mwanamke naye ambaye mtu mume amelala naye kwa shahawa, wote wawili wataoga majini, nao watakuwa najisi hata jioni. 19 Mwanamke ye yote, kama anatokwa na kitu, na kitu chake alichokuwa nacho mwilini mwake ni damu, ataketi katika kutengwa kwake muda wa siku saba; na mtu ye yote atakayemgusa atakuwa najisi hata jioni. 20 Na kitu cho chote akilaliacho katika kutengwa kwake kitakuwa najisi; na kila kitu ambacho akiketia kitakuwa najisi. 21 Mtu ye yote atakayekigusa kitanda chake huyo mwanamke atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 22 Mtu ye yote atakayekigusa cho chote ambacho huyo mwanamke amekiketia atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 23 Kwamba ni katika kitanda, au cho chote alichokikalia huyo mwanamke, atakapokigusa kitu hicho, atakuwa najisi hata jioni. 24 Na mtu ye yote atakayelala na mwanamke na unajisi ukawa juu yake, atakuwa najisi muda wa siku saba; na kila kitanda alichokilalia kitakuwa najisi. 25 Na mwanamke kama akitokwa na damu yake siku nyingi, nayo si katika majira ya kutengwa kwake, au kama anatoka damu kuzidi majira ya kutengwa kwake; siku hizo zote za kutoka damu ya unajisi wake, atakuwa kama alivyokuwa katika siku za kutengwa kwake; yeye yu najisi. 26 Kila kitanda akilaliacho katika siku zote za kutoka damu kitakuwa kama kitanda cha kutengwa kwake; na kila kitu atakachokilalia kitakuwa najisi, kama unajisi wa kutengwa kwake. 27 Na mtu ye yote atakayevigusa vitu vile atakuwa najisi, naye atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 28 Lakini huyo mwanamke kwamba ametakaswa na kule kutoka damu kwake, ndipo atakapojihesabia siku saba, na baadaye atakuwa safi. 29 Siku ya nane atajipatia hua wawili, au makinda mawili ya njiwa, na kumletea kuhani, mlangoni pa hema ya kukutania. 30 Kuhani atamsongeza mmoja kuwa sadaka ya dhambi, na wa pili kuwa sadaka ya kuteketezwa; naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake mbele za Bwana, kwa ajili ya kutoka damu ya unajisi kwake. 31 Ni hivi mtakavyowatenga wana wa Israeli na unajisi wao; ili wasife katika unajisi wao, hapo watakapoitia unajisi maskani yangu iliyo katikati yao. 32 Hii ndiyo sheria ya mwenye kisonono, na ya mtu ambaye shahawa yake yamtoka, akawa na unajisi kwa hiyo; 33 na ya mwanamke ambaye yu katika kutengwa kwake, na ya mtu ambaye ana kisonono, kama ni mtu mume, kama ni mtu mke, na ya huyo alalaye na mwanamke mwenye unajisi.

Mambo ya Walawi 16

1 Bwana akasema na Musa, baada ya kufa kwa hao wana wawili wa Haruni, walipokaribia mbele za Bwana, wakafa; 2 Bwana akamwambia Musa, Sema na Haruni ndugu yako, kwamba asiingie wakati wo wote katika mahali patakatifu ndani ya pazia, mbele ya kiti cha rehema, kilicho juu ya sanduku, asije akafa; maana, mimi nitaonekana katika lile wingu juu ya kiti cha rehema. 3 Haruni ataingia katika patakatifu na vitu hivi; ng'ombe mume mchanga kwa sadaka ya dhambi, na kondoo mume kwa sadaka ya kuteketezwa. 4 Ataivaa ile kanzu takatifu ya kitani, atakuwa na zile suruali za kitani mwilini mwake, atafungwa ule mshipi wa kitani, naye atavaa ile kofia ya kitani; hayo ndiyo mavazi matakatifu, naye ataoga mwili wake majini, na kuyavaa. 5 Kisha atatwaa mikononi mwa mkutano wa Waisraeli mbuzi waume wawili, kwa sadaka ya dhambi; na kondoo mume kwa sadaka ya kuteketezwa. 6 Na Haruni atamtoa yule ng'ombe wa sadaka ya dhambi, aliye kwa ajili ya nafsi yake, na kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, na kwa ajili ya nyumba yake. 7 Kisha atawatwaa wale mbuzi wawili na kuwaweka mbele za Bwana mlangoni pa hema ya kukutania. 8 Na Haruni atapiga kura juu ya wale mbuzi wawili; kura moja kwa ajili ya Bwana; na kura ya pili kwa ajili ya Azazeli. 9 Na Haruni atamleta yule mbuzi aliyeangukiwa na kura kwa ajili ya Bwana, na kumtoa awe sadaka ya dhambi. 10 Bali yule mbuzi aliyeangukiwa na kura kwa ajili ya Azazeli atawekwa hai mbele za Bwana ili kumfanyia upatanisho, ili kumpeleka jangwani kwa ajili ya Azazeli. 11 Na Haruni atamsongeza ng'ombe wa sadaka ya dhambi, aliye kwa ajili ya nafsi yake, na kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, na kwa ajili ya nyumba yake; naye atamchinja yule ng'ombe wa sadaka ya dhambi, aliye kwa ajili ya nafsi yake. 12 Kisha atatwaa chetezo kilichojaa makaa ya moto yatokayo katika madhabahu iliyo mbele za Bwana, na konzi mbili za uvumba mzuri uliopondwa sana, mikononi mwake, naye atauleta ndani ya pazia. 13 Kisha atatia ule uvumba juu ya moto mbele za Bwana, ili moshi wa ule uvumba ukisitiri kiti cha rehema kilicho juu ya ushuhuda, asije akafa. 14 Kisha atatwaa baadhi ya damu ya yule ng'ombe, na kuinyunyiza kwa kidole chake juu ya kiti cha rehema upande wa mashariki; na mbele ya kiti cha rehema atainyunyiza ile damu kwa kidole chake mara saba. 15 Kisha atamchinja yule mbuzi wa sadaka ya dhambi, aliye kwa ajili ya watu, na kuileta damu yake ndani ya pazia, na kwa damu hiyo atafanya vile vile kama alivyofanya kwa damu ya ng'ombe, na kuinyunyiza juu ya kiti cha rehema, na mbele ya kiti cha rehema, 16 naye atafanya upatanisho kwa ajili ya mahali patakatifu, kwa sababu ya mambo machafu ya wana wa Israeli, na kwa sababu ya makosa yao, naam, kwa ajili ya dhambi zao zote; naye atafanya vile vile kwa ajili ya hema ya kukutania, ikaayo pamoja nao katikati ya machafu yao. 17 Wala hapatakuwa na mtu katika hema ya kukutania, wakati aingiapo ili kufanya upatanisho katika patakatifu, hata atakapotoka nje, baada ya kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, na kwa ajili ya nyumba yake, na kwa ajili ya mkutano wote wa Israeli. 18 Kisha atatoka na kuiendea madhabahu iliyo mbele za Bwana na kufanya upatanisho kwa ajili yake; atatwaa baadhi ya damu ya yule ng'ombe, na ya damu ya yule mbuzi, na kuitia juu ya pembe za madhabahu pande zote. 19 Tena atanyunyiza baadhi ya damu juu ya madhabahu kwa kidole chake mara saba, na kuitakasa, ili machafu yote ya wana wa Israeli yaitoke. 20 Naye akiisha kufanya upatanisho kwa ajili ya mahali patakatifu, na hema ya kukutania, na madhabahu, atamleta yule mbuzi aliye hai. 21 Na Haruni ataweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha yule mbuzi aliye hai, na kuungama juu yake uovu wote wa wana wa Israeli, na makosa yao, naam, dhambi zao zote; naye ataziweka juu ya kichwa chake yule mbuzi, kisha atampeleka aende jangwani kwa mkono wa mtu aliye tayari. 22 Na yule mbuzi atachukua juu yake uovu wao wote, mpaka nchi isiyo watu; naye atamwacha mbuzi jangwani. 23 Na Haruni ataingia katika hema ya kukutania, naye atavua mavazi yake ya kitani, aliyoyavaa alipoingia katika patakatifu, atayaacha humo; 24 naye ataosha mwili wake kwa maji mahali patakatifu, na kuvaa nguo zake, na kutoka, na kusongeza sadaka ya kuteketezwa yake mwenyewe, na sadaka ya kuteketezwa ya watu, naye atafanya upatanisho kwa ajili ya nafsi yake, na kwa ajili ya watu. 25 Na mafuta ya sadaka ya dhambi atayateketeza juu ya madhabahu. 26 Na mtu yule amwachaye mbuzi wa Azazeli aende zake, ataosha nguo zake, na kuosha mwili wake kwa maji, na baadaye ataingia katika marago. 27 Na yule ng'ombe wa sadaka ya dhambi, na yule mbuzi wa sadaka ya dhambi, ambao damu yao ililetwa ndani ifanye ukumbusho katika patakatifu, watachukuliwa nje ya marago; nao watachoma moto ngozi zao, na nyama yao, na mavi yao. 28 Na yeye awachomaye moto atafua nguo zake, na kuosha mwili wake kwa maji, na baadaye ataingia maragoni. 29 Amri hii itakuwa amri ya milele kwenu; katika mwezi wa saba, siku ya kumi ya mwezi, mtajitaabisha roho zenu, msifanye kazi ya namna yo yote, mzalia na mgeni akaaye kati yenu. 30 Kwa maana siku hiyo upatanisho utafanywa kwa ajili yenu, ili kuwatakasa; nanyi mtatakaswa na dhambi zenu zote mbele za Bwana. 31 Ni Sabato ya raha ya makini kwenu nanyi mtajitaabisha roho zenu; ni amri ya milele. 32 Na kuhani atakayetiwa mafuta na kuwekwa wakfu badala ya baba yake, ataufanya huo upatanisho, naye atayavaa mavazi ya kitani, yaani, yale mavazi matakatifu. 33 Naye atafanya upatanisho kwa ajili ya patakatifu, naye atafanya upatanisho kwa ajili ya hema ya kukutania, na kwa ajili ya madhabahu; naye atafanya upatanisho kwa ajili ya makuhani, na kwa ajili ya watu wote wa kusanyiko. 34 Na amri hii itakuwa amri ya milele kwenu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya wana wa Israeli kwa sababu ya dhambi zao zote, mara moja kila mwaka. Naye akafanya vile vile kama Bwana alivyomwamuru Musa.

Mambo ya Walawi 17

1 Bwana akamwambia Musa, akisema, 2 Sema na Haruni, na wanawe, na wana wote wa Israeli, ukawaambie; Neno hili ndilo aliloliamuru Bwana, akisema, 3 Mtu awaye yote wa nyumba ya Israeli atakayechinja ng'ombe, au mwana-kondoo, au mbuzi, ndani ya marago, au atakayemchinja nje ya marago, 4 wala hamleti mlangoni pa hema ya kukutania, ili amtoe kuwa matoleo kwa Bwana mbele ya hema ya Bwana; mtu huyo atahesabiwa kuwa ana hatia ya damu; amemwaga damu; na mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake; 5 ili kusudi wana wa Israeli walete sadaka zao, wazichinjazo mashambani, naam, wazilete kwa Bwana, mpaka mlango wa hema ya kukutania, kwa huyo kuhani, ili wazichinje ziwe sadaka za amani kwa Bwana. 6 Naye kuhani atainyunyiza damu yake juu ya madhabahu ya Bwana, mlangoni pa hema ya kukutania, na kuyateketeza mafuta yake, yawe harufu njema mbele za Bwana. 7 Wala hawatatoa tena sadaka zao kwa wale majini, ambao huwafuata ili wafanye uasherati nao. Sheria hii itakuwa sheria ya milele kwao, kizazi baada ya kizazi. 8 Nawe utawaambia, Mtu awaye yote katika nyumba ya Israeli, au miongoni mwa wageni, wanaokaa nao, atoaye sadaka ya kuteketezwa au dhabihu, 9 wala haileti mlangoni pa hema ya kukutania, ili aisongeze kwa Bwana basi mtu huyo atatengwa na watu wake. 10 Kisha mtu awaye yote wa nyumba ya Israeli, au miongoni mwa hao wageni wakaao kati yao, atakayekula damu, ya aina yo yote, nitakunja uso wangu juu ya mtu huyo alaye damu, nami nitamkatilia mbali na watu wake. 11 Kwa kuwa uhai wa mwili u katika hiyo damu; nami nimewapa ninyi hiyo damu juu ya madhabahu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu; kwani ni hiyo damu ifanyayo upatanisho kwa sababu ya nafsi. 12 Kwa hiyo naliwaambia wana wa Israeli, Hapana mtu miongoni mwenu aliye na ruhusa kula damu, wala mgeni aketiye kati yenu asile damu. 13 Mtu ye yote aliye wa wana wa Israeli, au wa hao wageni wakaao kati yenu, ambaye amemshika mnyama, au ndege ambaye huliwa, katika kuwinda kwake; atamwaga damu yake, na kuifunika mchanga. 14 Kwa maana kuliko huo uhai wa mnyama, hiyo damu yake ni moja na uhai wake; kwa hiyo naliwaambia wana wa Israeli, Msile damu ya mnyama wa aina yo yote; kwa kuwa uhai wa wanyama wote ni katika hiyo damu yake; atakayeila awaye yote atakatiliwa mbali. 15 Tena kila mtu atakayekula nyamafu, au nyama aliyeraruliwa na wanyama, kama ni mzalia, kama ni mgeni, atafua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni; ndipo atakapokuwa safi. 16 Lakini kwamba hazifui, wala haogi mwili, ndipo atakapochukua uovu wake.

Mambo ya Walawi 18

1 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena wewe na wana wa Israeli, uwaambie, Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 3 Nanyi msifanye matendo kama yale ya nchi ya Misri mliyokaa; wala msifanye matendo kama yale ya nchi ya Kanaani, nitakayowapeleka; wala msiende katika amri zao hao. 4 Mtazifanya hukumu zangu, nanyi mtazishika amri zangu, ili mwenende katika hizo; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 5 Kwa ajili ya hayo mtazishika amri zangu na hukumu zangu; ambazo mtu akizitumia ataishi kwa hizo; mimi ndimi Bwana. 6 Mtu ye yote aliye wa kwenu asimkaribie mwenziwe aliye wa jamaa yake ya karibu ili kumfunua utupu; mimi ndimi Bwana. 7 Utupu wa baba yako, wala utupu wa mama yako, usifunue, maana ndiye mama yako; usifunue utupu wake. 8 Utupu wa mke wa baba yako, usifunue; maana, ni utupu wa baba yako. 9 Utupu wa umbu lako, binti ya baba yako, au binti ya mama yako, kwamba alizaliwa nyumbani mwenu au kwamba alizaliwa kwengine, utupu wa hao usifunue. 10 Utupu wa binti ya mwanao mume, au wa binti ya binti yako, utupu wao hao usifunue; kwa kuwa ndio utupu wako mwenyewe. 11 Utupu wa binti ya mkewe baba yako, aliyezaliwa na baba yako, yeye ni umbu lako, usifunue utupu wake. 12 Usifunue utupu wa umbu lake baba yako; maana, yeye ni jamaa aliye karibu. 13 Usifunue utupu wa umbu la mama yako; maana, yeye ni jamaa ya mama yako ya karibu. 14 Usifunue utupu wa ndugu ya baba yako, usimkaribie mkewe huyo; yeye ni shangazi lako. 15 Usifunue utupu wa mkweo mwanamke; yeye ni mke wa mwanao; usifunue utupu wake huyo. 16 Usifunue utupu wa mke wa nduguyo; maana, ni utupu wa nduguyo. 17 Usifunue utupu wa mwanamke na binti yake; usimtwae binti ya mwanawe mume, au binti ya binti yake, ili kufunua utupu wake; hao ni jamaa ya karibu; ni uovu mkuu. 18 Wala usitwae mwanamke pamoja na nduguye, awe mtesi wake, na kufunua utupu wake, huyo wa pili atakapokuwa yu hai. 19 Nawe usimkaribie mwanamke kufunua utupu wake wakati wa kutengwa kwa ajili ya unajisi wake. 20 Usilale na mke wa mwenzio, ukajitia unajisi naye. 21 Nawe usitoe kizazi chako cho chote na kuwapisha kwa Moleki, wala usilinajisi jina la Mungu wako; mimi ndimi Bwana. 22 Usilale na mwanamume mfano wa kulala na mwanamke; ni machukizo. 23 Wala usilale na mnyama ye yote, ili kujitia unajisi kwake; wala mwanamke asisimame mbele ya mnyama ili kulala naye; ni uchafuko. 24 Msijitie unajisi katika mambo hayo hata mojawapo; kwa maana hizo taifa nitakazozitoa mbele zenu zimekuwa najisi kwa mambo hayo yote; 25 na hiyo nchi imekuwa najisi; kwa ajili ya hayo naipatiliza uovu wake juu yake, na hiyo nchi yatapika wenyeji wake na kuwatoa. 26 Kwa hiyo mtazishika amri zangu na hukumu zangu, wala msifanye machukizo hayo mojawapo; yeye aliye mzalia, wala mgeni aketiye kati yenu; 27 (kwa kuwa hao watu wa nchi wameyafanya machukizo haya yote, hao waliotangulia mbele zenu, na hiyo nchi imekuwa najisi;) 28 ili kwamba hiyo nchi isiwatapike na ninyi pia, hapo mtakapoitia unajisi, kama ilivyoitapika hiyo taifa iliyotangulia mbele yenu. 29 Kwani mtu awaye yote atakayefanya machukizo hayo mojawapo, nafsi hizo zitakazoyafanya zitakatiliwa mbali na watu wao. 30 Kwa ajili ya hayo yashikeni mausia yangu, ili kwamba msifanye kabisa desturi hizi zichukizazo mojawapo, zilizotangulia kufanywa mbele zenu, wala msijitie unajisi katika mambo hayo; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.

Mambo ya Walawi 19

1 Bwana akanena na Musa, akamwambia, 2 Nena na mkutano wote wa wana wa Israeli, uwaambie, Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana, Mungu wenu, ni mtakatifu. 3 Kila mtu na amche mama yake, na baba yake, nanyi mtazitunza Sabato zangu; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 4 Msigeuke kuandama sanamu, wala msijifanyizie miungu ya kusubu mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 5 Nanyi hapo mtakapomchinjia Bwana sadaka ya amani mtaisongeza ili kwamba mpate kukubaliwa. 6 Italiwa siku iyo hiyo mliyoichinja, na siku ya pili yake; na kama kitu cho chote katika sadaka hiyo kilisalia hata siku ya tatu kitachomwa moto. 7 Kwamba sadaka hiyo yaliwa hata kidogo siku ya tatu ni machukizo; haitakubaliwa; 8 lakini kila mtu atakayekula atauchukua uovu wake mwenyewe, kwa sababu amekinajisi kitu hicho kitakatifu cha Bwana; na nafsi hiyo itakatiliwa mbali na watu wake. 9 Na mtakapovuna mavuno ya nchi yenu, usivune kabisa kabisa pembe za shamba lako, wala usiyakusanye masazo ya mavuno yako; 10 wala usiyakusanye masazo ya mizabibu yako, wala usiyaokote matunda ya mizabibu yako yaliyopukutika; uyaache kwa ajili ya maskini na mgeni; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 11 Msiibe, wala msidanganye, wala msiambiane uongo. 12 Msiape uongo kwa jina langu, hata ukalinajisi jina la Mungu wako; Mimi ndimi Bwana. 13 Usimdhulumu jirani yako, wala kumnyang'anya mali yake; ijara yake aliyeajiriwa isikae kwako usiku kucha hata asubuhi. 14 Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi Bwana. 15 Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki. 16 Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; mimi ndimi Bwana. 17 Usimchukie ndugu yako moyoni mwako; ni lazima kumkemea jirani yako, wala usichukue dhambi kwa ajili yake. 18 Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako kama nafsi yako; Mimi ndimi Bwana. 19 Mtazishika amri zangu. Usiwaache wanyama wako wa mfugo wakazaana kwa namna mbalimbali; usipande shamba lako mbegu za namna mbili pamoja; wala usivae mwilini mwako nguo ya namna mbili zilizochanganywa pamoja. 20 Tena mtu ye yote alalaye na mwanamke aliye mjakazi, naye ameposwa na mume, wala hakukombolewa kwa lo lote, wala hakupewa uhuru; wataadhibiwa; hawatauawa, kwa sababu huyo mwanamke hakuwa huru. 21 Na huyo mume ataleta sadaka yake ya hatia aitoe kwa Bwana, hata mlangoni pa hema ya kukutania; kondoo mume kwa hiyo sadaka ya hatia. 22 Kisha huyo kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake, kwa huyo kondoo mume wa sadaka ya hatia mbele za Bwana, kwa ajili ya dhambi yake aliyoifanya; naye atasamehewa hiyo dhambi yake aliyoifanya. 23 Nanyi hapo mtakapoingia nchi ile, mkiwa mmepanda miti ya namna zote kwa ajili ya chakula, ndipo mtayahesabu matunda yake kama ni kutotahiriwa; muda wa miaka mitatu miti hiyo itakuwa kwenu kama kutotahiriwa; matunda yake hayataliwa. 24 Lakini mwaka wa nne matunda yake yote yatakuwa ni matakatifu, kwa ajili ya kumpa Bwana shukrani. 25 Na katika mwaka wa tano mtakula katika matunda yake, ili ipate kuwapa maongeo yake; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 26 Msile kitu cho chote pamoja na damu yake; wala msifanye kuloga, wala kutumia utambuzi. 27 Msinyoe denge pembe za vichwani, wala msiharibu pembe za ndevu zenu. 28 Msichanje chale yo yote katika nyama ya miili yenu kwa ajili ya wafu, wala msiandike alama miilini mwenu; mimi ndimi Bwana. 29 Usimnajisi binti yako, ili kumfanya awe kahaba; isiwe hiyo nchi kuuandama ukahaba, na nchi kujawa na uovu mkuu. 30 Zishikeni Sabato zangu, mpaheshimu patakatifu pangu; mimi ndimi Bwana. 31 Msiwaendee wenye pepo, wala wachawi; msiwatafute; ili kutiwa unajisi na wao; Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 32 Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee; nawe mche Mungu wako, Mimi ndimi Bwana. 33 Na mgeni akikaa pamoja nawe katika nchi yako, usimdhulumu. 34 Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri; Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 35 Msifanye yasiyo haki katika hukumu, wala katika kupima, wala katika mizani, wala katika cheo. 36 Mizani ya haki, vipimo vya haki, efa ya haki, hini ya haki, ndivyo mtakavyokuwa navyo. Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, niliyewatoa katika nchi ya Misri. 37 Zishikeni sheria zangu, na hukumu zangu, na kuzitenda. Mimi ndimi Bwana.

Mambo ya Walawi 20

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Tena uwaambie wana wa Israeli, Mtu awaye yote miongoni mwa wana wa Israeli, au miongoni mwa wageni waketio katika Israeli, atakayetoa katika kizazi chake na kumpa Moleki, sharti atauawa; wenyeji wa nchi watampiga kwa mawe. 3 Mimi nami nitamkazia uso wangu mtu huyo, nami nitamkatilia mbali na watu wake; kwa kuwa ametoa katika kizazi chake na kumpa Moleki, ili kupatia unajisi patakatifu pangu, na kulinajisi jina langu takatifu. 4 Tena kama wenyeji wa nchi wakimfumbia macho mtu huyo kwa njia yo yote, hapo atoapo katika kizazi chake na kumpa Moleki, wasimwue; 5 ndipo mimi nitamkazia uso wangu mtu huyo, na jamaa zake, nami nitamkatilia mbali, na hao wote wamwandamao katika uzinifu, ili kufanya uzinifu pamoja na Moleki, watengwe mbali na watu wao. 6 Na mtu yule atakayewaendea wenye pepo, na wachawi, ili kuzini pamoja nao, nitakaza uso wangu juu ya mtu yule, nitamtenga na watu wake. 7 Jitakaseni basi, iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 8 Nanyi zishikeni sheria zangu, na kuzitenda; Mimi ndimi Bwana niwatakasaye ninyi. 9 Kwa maana kila mtu amlaaniye baba yake au mama yake hakika atauawa, amemlaani baba yake na mama yake; damu yake itakuwa juu yake. 10 Na mtu aziniye na mke wa mtu mwingine, naam, yeye aziniye na mke wa jirani yake, mtu mume aziniye, na mwanamke aziniye, hakika watauawa. 11 Na mtu mume atakayelala pamoja na mke wa baba yake amefunua utupu wa baba yake; wote wawili hakika watauawa; damu yao itakuwa juu yao. 12 Na mtu mume akilala na mkwewe mwanamke wote wawili hakika watauawa; wamefanya yaliyo uchafuko; damu yao itakuwa juu yao. 13 Tena mtu mume akilala pamoja na mtu mume, kama alalavyo na mtu mke, wote wawili wamefanya machukizo; hakika watauawa; damu yao itakuwa juu yao. 14 Tena mtu mume akimwoa mke pamoja na mama yake, ni uovu mkuu; watachomwa moto, yeye mume na hao wanawake pia; ili kwamba usiwe uovu kati yenu. 15 Tena mtu mume akilala na mnyama, hakika atauawa; nanyi mtamwua huyo mnyama. 16 Tena mwanamke akimkaribia mnyama ye yote, na kulala pamoja naye, mtamwua huyo mwanamke, na mnyama pia; hakika watauawa; damu yao itakuwa ni juu yao. 17 Tena mtu mume akimwoa umbu lake, binti ya baba yake, au binti ya mama yake, na kuuona utupu wake, na huyo mwanamke kauona utupu wake huyo mume; ni jambo la aibu; watakatiliwa mbali mbele ya macho ya wana wa watu wao; amefunua utupu wa umbu lake; naye atauchukua uovu wake. 18 Tena mtu mume akilala na mwanamke aliye na ugonjwa wake, na kufunua utupu wake; amelifunua jito la damu yake, naye mwanamke amefunua jito la damu yake; wote wawili watakatiliwa mbali na watu wao. 19 Usifunue utupu wa umbu la mama yako, wala umbu la baba yako; kwa kuwa huyo amefunua utupu wa jamaa yake ya karibu; watauchukua uovu wao. 20 Tena mtu mume akilala na mke wa mjomba wake, ameufunua utupu wa mjomba wake; watauchukua uovu wao; watakufa bila kuzaa mwana. 21 Tena mtu mume akimtwaa mke wa nduguye, ni uchafu; ameufunua utupu wa nduguye; hao watakuwa hawana wana. 22 Basi zishikeni amri zangu zote, na hukumu zangu zote, na kuzifanya; ili kwamba hiyo nchi, ambayo nawapeleka ninyi kukaa, isiwatapike. 23 Nanyi msiende kwa kuziandama desturi za taifa, niitoayo mbele yenu; kwa kuwa wao waliyafanya mambo hayo yote, na kwa ajili ya hayo niliwachukia. 24 Lakini mimi nimewaambia ninyi, Mtairithi nchi yao, nami nitawapa ninyi kuimiliki; nchi iliyojaa maziwa na asali; mimi ni Bwana, Mungu wenu, niliyewatenga ninyi na mataifa. 25 Kwa ajili ya hayo mtapambanua kati ya mnyama aliye safi na mnyama aliye najisi, na kati ya ndege aliye tohara na ndege aliye najisi; nanyi msizifanye nafsi zenu kuwa machukizo kwa njia ya mnyama, au kwa njia ya ndege, au kwa njia ya kitu cho chote ambacho nchi imejaa nacho, niliowatenga nanyi kuwa ni najisi. 26 Nanyi mtakuwa watakatifu kwangu mimi; kwa kuwa mimi Bwana ni mtakatifu nami nimewatenga ninyi na mataifa, ili kwamba mwe wangu. 27 Tena mtu mume au mtu mke aliye na pepo, au aliye mchawi, hakika atauawa; watawapiga kwa mawe; damu yao itakuwa juu yao.

Mambo ya Walawi 21

1 Kisha Bwana akamwambia Musa, Nena na hao makuhani, wana wa Haruni, uwaambie, Mtu asijinajisi kwa ajili ya wafu katika watu wake; 2 isipokuwa ni kwa ajili ya jamaa yake wa karibu, kwa ajili ya mama yake, na kwa ajili baba yake, na kwa ajili ya mwanawe, na kwa ajili ya binti yake, na kwa ajili ya nduguye mwanamume; 3 na kwa ajili ya umbu lake aliye mwanamwali, aliye wa udugu kwake, ambaye hajaolewa na mume; ana ruhusa kujitia unajisi kwa ajili yake huyo. 4 Asijitie unajisi, ijapokuwa ni mkubwa katika watu wake, hata akajinajisi. 5 Wasijifanyie upaa kichwani, wala wasinyoe pembe za ndevu zao, wala wasichanje chale katika miili yao. 6 Watakuwa watakatifu kwa Mungu wao, wala wasilinajisi jina la Mungu wao; kwa kuwa wao ndio wasongezao sadaka za Bwana kwa njia ya moto, chakula cha Mungu wao; kwa ajili ya hayo watakuwa watakatifu. 7 Wasimwoe mwanamke aliye kahaba, au huyo aliye mwenye unajisi; wala wasimwoe mwanamke aliyeachwa na mumewe; kwa kuwa yeye kuhani ni mtakatifu kwa Mungu wake. 8 Kwa hiyo basi utamtakasa; kwa kuwa yeye husongeza chakula cha Mungu wako; atakuwa mtakatifu kwako wewe; kwa kuwa mimi Bwana niwatakasaye ninyi ni mtakatifu. 9 Na binti ya kuhani ye yote atakapojitia unajisi kwa ukahaba, amemtia unajisi baba yake; atachomwa moto. 10 Na yeye aliye kuhani mkuu katika nduguze, ambaye mafuta ya kutiwa yamemiminwa kichwani mwake, naye akawekwa wakfu ili ayavae hayo mavazi, yeye hataziacha wazi nywele za kichwa chake, wala hatazirarua nguo zake; 11 wala hataingia penye maiti, wala asijitie unajisi kwa ajili ya baba yake wala mama yake; 12 wala asitoke katika mahali patakatifu, wala asipatie unajisi mahali patakatifu pa Mungu wake; kwa kuwa utakaso wa hayo mafuta ya kutiwa ya Mungu wake u juu yake; mimi ndimi Bwana. 13 Naye atamwoa mwanamke katika ubikira wake. 14 Asitwae mjane, wala mwanamke aliyeachwa na mumewe, wala mwanamke mwenye unajisi, wala kahaba; lakini atamwoa mwanamwali katika watu wake mwenyewe. 15 Naye asiwatie unajisi kizazi chake katika watu wake; kwa kuwa mimi ndimi Bwana nimtakasaye. 16 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 17 Nena na Haruni, umwambie, Mtu awaye yote wa kizazi chako wewe katika vizazi vyao, aliye na kilema, asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake. 18 Kwa kuwa mtu awaye yote aliye na kilema hatakaribia; mtu kipofu, au kiwete, au mtu aliye na pua iliyoharibika, au aliye na kitu kilichozidi vimpasavyo mwili, 19 au mtu aliyevunjika mguu, au aliyevunjika mkono, 20 au aliye na kijongo, au aliye kibeti, au aliye na kilema cha jichoni, au aliye na upele, au mwenye buba, au aliyevunjika mapumbu; 21 mtu awaye yote wa kizazi cha Haruni kuhani aliye na kilema asikaribie kuzisongeza sadaka za Bwana kwa njia ya moto; ana kilema huyo asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake. 22 Atakula chakula cha Mungu wake, katika hicho kilicho kitakatifu sana, na hicho kilicho kitakatifu. 23 Lakini hataingia ndani ya pazia, wala asikaribie madhabahu, kwa sababu ana kilema; ili kwamba asipanajisi patakatifu pangu; kwa kuwa mimi ndimi Bwana niwatakasaye. 24 Basi Musa akanena na Haruni na wanawe, na wana wa Israeli wote.

Mambo ya Walawi 22

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na Haruni na wanawe, ili wajitenge wenyewe na vitu vitakatifu vya wana wa Israeli ambavyo wanitakasia mimi, tena kwamba wasilinajisi jina langu takatifu; mimi ndimi Bwana. 3 Waambie, Mtu ye yote wa kizazi chenu chote katika vizazi vyenu, atakayevikaribia vile vitu vitakatifu, ambavyo wana wa Israeli wamtakasia Bwana, naye ana unajisi, mtu huyo atakatiliwa mbali asiwe mbele zangu; mimi ndimi Bwana. 4 Mtu ye yote wa kizazi cha Haruni aliye mwenye ukoma, au mwenye kisonono; yeye asile katika vitu vitakatifu, hata atakapokuwa safi. Tena mtu awaye yote atakayekinusa kitu kilicho na unajisi kwa sababu ya wafu, au mtu ambaye shahawa humtoka; 5 au mtu amgusaye mnyama atambaaye, wa kumpatia unajisi, au kwamba amgusa mtu wa kumpatia unajisi, kwa unajisi wo wote alio nao; 6 huyo mtu atakayegusa kitu cho chote namna hiyo atakuwa najisi hata jioni, naye hatakula katika vitu vitakatifu, asipooga mwili wake majini. 7 Jua likiisha kuchwa atakuwa safi; kisha baadaye atakula katika vitu vitakatifu, maana ni chakula chake. 8 Nyamafu au mnyama aliyeraruliwa na wanyama asile, asijitie unajisi kwa hiyo nyama; mimi ndimi Bwana. 9 Basi kwa hiyo watayashika mausia yangu, wasije wakachukua dhambi kwa hayo, nao wakafa humo, wakiyanajisi; mimi ndimi Bwana niwatakasaye. 10 Mgeni awaye yote asile katika kitu kitakatifu; mgeni wa kuhani akaaye kwake, au mtumishi aliyeajiriwa, asile katika kitu kitakatifu. 11 Lakini kwamba kuhani akinunua mtu ye yote, kwa kumnunua kwa fedha zake, yeye atakula katika hicho; na hao waliozaliwa nyumbani mwake watakula katika chakula chake. 12 Na binti ya kuhani kwamba ameolewa na mgeni, asile katika sadaka ya kuinuliwa katika vitu vile vitakatifu. 13 Lakini kwamba binti ya kuhani ni mjane, au kwamba ameachwa na mumewe, wala hana mtoto, kisha amerudi na kuketi katika nyumba ya baba yake, kama vile katika ujana wake, yeye atakula katika chakula cha baba yake; lakini mgeni awaye yote asile katika chakula hicho. 14 Tena kama mtu ye yote akila katika kitu kilicho kitakatifu pasipo kukijua, ndipo ataongeza sehemu ya tano juu ya kitu hicho, na kumpa kuhani kitu hicho kitakatifu. 15 Wala wasivinajisi vitu vitakatifu vya wana wa Israeli, wavisongezavyo kwa Bwana; 16 hata wakawatwika ule uovu uletao hatia, hapo walapo vitu vyao vitakatifu; kwa kuwa mimi ndimi Bwana niwatakasaye. 17 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 18 Nena na Haruni na wanawe, na wana wa israeli wote, uwaambie, Mtu ye yote wa nyumba ya Israeli, au wa wageni walio katika Israeli, atakayetoa matoleo yake, kama ni nadhiri zao mojawapo, au kama ni sadaka yo yote ya hiari, watakayomtolea Bwana kuwa sadaka ya kuteketezwa; 19 ili mpate kukubaliwa, mtaleta mume mkamilifu, katika ng'ombe, au katika kondoo, au katika mbuzi. 20 Lakini mnyama ye yote aliye na kilema msimtoe; kwa kuwa hatakubaliwa kwa ajili yenu. 21 Na mtu awaye yote atakayemtolea Bwana dhabihu katika sadaka za amani, ili kuondoa nadhiri, au sadaka ya moyo wa kupenda, katika ng'ombe, au katika kondoo, atakuwa mkamilifu, apate kukubaliwa; pasiwe na kilema ndani yake cho chote. 22 Kipofu, au aliyevunjika mahali, au kiwete au aliye na vidonda, au aliye na upele, au aliye na kikoko, hamtamtolea Bwana wanyama hao, wala msiwasongeze kwa Bwana kwa njia ya moto juu ya madhabahu. 23 Ng'ombe, au mwana-kondoo aliye na kitu kilichozidi, au aliyepungukiwa na kitu katika vitu vya mwilini mwake, mna ruhusa kutoa kuwa sadaka ya moyo wa kupenda; lakini kwa ajili ya nadhiri hatakubaliwa. 24 Mnyama aliyeumia mapumbu yake, au kusetwa, au kuvunjwa, au kukatwa, msimtolee Bwana; wala msifanye hivi katika nchi yenu. 25 Wala msisongeze chakula cha Mungu wenu katika wanyama hao mmojawapo kitokacho mkononi mwa mgeni; kwa sababu uharibifu wao u ndani yao, wana kilema ndani yao; hawatakubaliwa kwa ajili yenu. 26 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 27 Hapo ng'ombe, au kondoo, au mbuzi, akizaliwa, atakuwa pamoja na mamaye muda wa siku saba; na siku ya nane na baadaye atakubaliwa kuwa ni sadaka ya kutolewa kwa Bwana kwa njia ya moto. 28 Tena kama ni ng'ombe, au kama ni kondoo, msimchinje huyo na mwanawe wote wawili kwa siku moja. 29 Tena mtakapomchinjia Bwana dhabihu ya shukrani, mtamchinja ili mpate kukubaliwa. 30 Italiwa siku iyo hiyo; msisaze kitu chake hata asubuhi; mimi ndimi Bwana. 31 Kwa hiyo mtayashika maagizo yangu, na kuyafanya; mimi ndimi Bwana. 32 Wala msilinajisi jina langu takatifu; lakini nitatakaswa mimi katika wana wa Israeli; mimi ndimi Bwana niwatakasaye ninyi, 33 niliyewaleta mtoke nchi ya Misri, ili niwe Mungu wenu; mimi ndimi Bwana.

Mambo ya Walawi 23

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Sikukuu za Bwana, ambazo mtazipigia mbiu kuwa ni makusanyiko matakatifu; hizi ni sikukuu zangu. 3 Mtafanya kazi siku sita; lakini siku ya saba ni Sabato ya kustarehe kabisa, kusanyiko takatifu; msifanye kazi ya namna yo yote; ni Sabato kwa Bwana katika makao yenu yote. 4 Sikukuu za Bwana ni hizi, ni makusanyiko matakatifu, ambayo mtayapigia mbiu kwa nyakati zake. 5 Mwezi wa kwanza, siku ya kumi na nne ya mwezi wakati wa jioni, ni pasaka ya Bwana. 6 Na siku ya kumi na tano ya mwezi ule ule ni sikukuu kwa Bwana ya mkate usiotiwa chachu; mtaila mikate isiyochachwa muda wa siku saba. 7 Siku ya kwanza mtakuwa na kusanyiko takatifu msifanye kazi yo yote ya utumishi. 8 Lakini mtasongeza sadaka kwa Bwana kwa njia ya moto siku saba; siku ya saba ni kusanyiko takatifu; msifanye kazi yo yote ya utumishi. 9 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 10 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Hapo mtakapokuwa mmekwisha ingia hiyo nchi niwapayo, na kuyavuna mavuno yake, ndipo mtakapomletea kuhani mganda wa malimbuko ya mavuno yenu; 11 naye atautikisa mganda mbele za Bwana ili kwamba ukubaliwe kwa ajili yenu; siku ya pili baada ya Sabato kuhani atautikisa. 12 Na siku hiyo mtakayoutikisa mganda, mtamsongeza mwana-kondoo wa kiume mkamilifu wa mwaka wa kwanza awe sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana. 13 Na sadaka yake ya unga itakuwa sehemu za kumi mbili za efa za unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, ni kafara iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto kuwa harufu ya kupendeza; na sadaka yake ya kinywaji itakuwa ni divai, robo ya hini. 14 Nanyi msile mkate, wala bisi, wala masuke machanga, hata siku iyo hiyo, hata mtakapokuwa mmekwisha kuleta sadaka ya Mungu wenu; hii ni amri ya milele katika vizazi vyenu katika makao yenu yote. 15 Nanyi mtajihesabia tangu siku ya pili baada ya Sabato, tangu siku hiyo mliyouleta mganda wa sadaka ya kutikiswa; zitatimia Sabato saba; 16 hata siku ya pili ya hiyo Sabato ya saba mtahesabu siku hamsini; nanyi mtamsongezea Bwana sadaka ya unga mpya. 17 Mtatoa katika makao yenu mikate miwili ya kutikiswa, itakuwa ya sehemu za kumi mbili za efa; itakuwa ya unga mwembamba, itaokwa na chachu, iwe malimbuko kwa Bwana. 18 Nanyi, pamoja na hiyo mikate, mtasongeza wana-kondoo saba, walio wakamilifu, wa mwaka wa kwanza, na ng'ombe mume mmoja, na kondoo waume wawili; watakuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana, pamoja na sadaka yao ya unga, na sadaka zao za kinywaji, sadaka ya harufu ya kupendeza iliyosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 19 Nanyi mtasongeza mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi, na wana-kondoo wawili waume wa mwaka wa kwanza kuwa dhabihu ya sadaka za amani. 20 Kisha kuhani atawatikisa pamoja na hiyo mikate ya malimbuko kuwa sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana, pamoja na wale wana-kondoo wawili; watakuwa watakatifu kwa Bwana, wawe wa huyo kuhani. 21 Nanyi mtapiga mbiu siku iyo hiyo; kutakuwa na kusanyiko takatifu kwenu; msifanye kazi yo yote ya utumishi; ni amri ya milele katika makao yenu yote, katika vizazi vyenu. 22 Nanyi hapo mtakapovuna mavuno ya nchi yenu, usivune kabisa kabisa pembe za shamba lako, wala msiyakusanye masazo ya mavuno yako; utayaacha kwa ajili ya huyo maskini, na mgeni; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 23 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 24 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mwezi wa saba, siku ya kwanza ya mwezi, kutakuwa na kustarehe kabisa kwenu, ni ukumbusho wa kuzipiga baragumu, ni kusanyiko takatifu. 25 Msifanye kazi yo yote ya utumishi; nanyi mtasongeza sadaka kwa Bwana kwa njia ya moto. 26 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 27 Lakini siku ya kumi ya mwezi huo wa saba ni siku ya upatanisho; itakuwa kusanyiko takatifu kwenu, nanyi mtazitesa nafsi zenu; nanyi mtasongeza sadaka kwa Bwana kwa njia ya moto. 28 Nanyi msifanye kazi yo yote siku hiyo; kwa kuwa ni siku ya upatanisho, ili kufanya upatanisho kwa ajili yenu mbele za Bwana, Mungu wenu. 29 Kwa kuwa mtu awaye yote asiyejitesa mwenyewe siku iyo hiyo, atakatiliwa mbali na watu wake. 30 Na mtu ye yote afanyaye kazi ya namna yo yote siku hiyo, mtu huyo nitamwangamiza atoke katika watu wake. 31 Msifanye kazi ya namna yo yote; ni amri ya milele katika vizazi vyenu, katika makao yenu yote. 32 Itakuwa kwenu sabato ya kustarehe kabisa, nanyi mtazitesa nafsi zenu; siku ya kenda ya mwezi wakati wa jioni, tangu jioni hata jioni, mtaishika hiyo Sabato yenu. 33 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 34 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Siku ya kumi na tano ya mwezi huo wa saba ni sikukuu ya vibanda muda wa siku saba kwa Bwana. 35 Siku ya kwanza kutakuwa na kusanyiko takatifu; msifanye kazi yo yote ya utumishi. 36 Mtamsongezea Bwana sadaka kwa moto siku saba; siku ya nane kutakuwa na kusanyiko takatifu kwenu; nanyi mtamsongezea Bwana sadaka kwa moto; ni mkutano wa makini huu; msifanye kazi yo yote ya utumishi. 37 Sikukuu za Bwana ni hizi, ambazo mtazipigia mbiu ya kuwa ni makusanyiko matakatifu, ili mmsongezee Bwana sadaka kwa moto, sadaka ya kuteketezwa, na sadaka ya unga, na dhabihu, na sadaka za kinywaji, kila sadaka kwa siku yake; 38 zaidi ya hizo Sabato za Bwana, na zaidi ya matoleo yenu, na zaidi ya hizo nadhiri zenu zote, na zaidi ya sadaka zenu za hiari, ambazo mwampa Bwana. 39 Lakini siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba, hapo mtakapokuwa mmekwisha kuyachuma mavuno ya nchi, mtaweka sikukuu ya Bwana muda wa siku saba; siku ya kwanza kutakuwa na kustarehe kabisa, na siku ya nane kutakuwa na kustarehe kabisa. 40 Nanyi siku ya kwanza mtajipatia matunda ya miti mizuri, na makuti ya mitende, na matawi ya miti minene, na mierebi ya vijitoni; nanyi mtafurahi mbele za Bwana, Mungu wenu, muda wa siku saba. 41 Nanyi mtaishika kuwa sikukuu kwa Bwana muda wa siku saba katika mwaka; ni amri ya milele katika vizazi vyenu; mtaishika katika mwezi wa saba. 42 Mtakaa katika vibanda muda wa siku saba; wazalia wote wa Israeli watakaa katika vibanda; 43 ili vizazi vyenu vipate kujua ya kuwa niliwaketisha wana wa Israeli katika vibanda, hapo nilipowaleta kutoka nchi ya Misri; mimi ndimi Bwana Mungu wenu. 44 Naye Musa akawaambia wana wa Israeli hizo sikukuu za Bwana.

Mambo ya Walawi 24

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Waagize wana wa Israeli kwamba wakuletee mafuta ya zeituni safi ya kupondwa kwa ajili ya ile nuru, ili hiyo taa iwake daima. 3 Hapo nje ya pazia la ushahidi, ndani ya hema ya kukutania, Haruni ataitengeza tangu jioni hata asubuhi mbele za Bwana daima; ni amri ya milele katika vizazi vyenu. 4 Atazitengeza hizo taa katika kile kinara kilicho safi mbele za Bwana daima. 5 Nawe utatwaa unga mwembamba, na kuoka mikate kumi na miwili ya huo unga; sehemu za kumi mbili za efa, zitakuwa katika mkate mmoja. 6 Nawe iweke mistari miwili, mikate sita kwa kila mstari, juu ya hiyo meza safi, mbele za Bwana. 7 Nawe utatia ubani safi juu ya kila mstari, ili uwe ukumbusho kwa hiyo mikate, sadaka ya kusongezwa kwa Bwana kwa moto. 8 Kila siku ya Sabato ataipanga mbele za Bwana daima; ni kwa ajili ya wana wa Israeli, agano la milele. 9 Nayo itakuwa ya Haruni na wanawe; nao wataila katika mahali patakatifu; kwa sababu kwake ni takatifu sana katika sadaka zisongezwazo kwa Bwana kwa moto, kwa amri ya milele. 10 Ikawa mwana wa mwanamke wa Kiisraeli, ambaye babaye alikuwa Mmisri, akatokea kati ya wana wa Israeli; na huyo mwana wa mwanamke wa Kiisraeli, na Mwisraeli mmoja, wakapigana pamoja ndani ya marago; 11 kisha huyo mwana wa mwanamke wa Kiisraeli akalikufuru hilo Jina, na kuapiza; nao wakamleta kwa Musa. Na jina la mamaye alikuwa akiitwa Shelomithi, binti ya Dibri, wa kabila ya Dani. 12 Nao wakamtia kifungoni, ili wapate kuambiwa neno litakalotoka kinywani pa Bwana. 13 Na Bwana akasema na Musa, na kumwambia, 14 Mtoe huyo aliyeapiza nje ya marago; na wale wote waliomsikia na waweke mikono yao kichwani mwake, kisha mkutano wote na wamwue kwa kumpiga kwa mawe. 15 Nawe nena na wana wa Israeli na kuwaambia, Mtu awaye yote atakayemlaani Mungu wake atachukua dhambi yake. 16 Na yeye atakayelikufuru jina la Bwana hakika atauawa; mkutano wote watamwua kwa kumpiga kwa mawe; kama ni mgeni, kama ni mzalia, hapo atakapolikufuru jina la Bwana atauawa. 17 Na mtu ampigaye mtu hata akafa, lazima atauawa; 18 na atakayempiga mnyama hata akafa atalipa; uhai kwa uhai. 19 Na mtu akimtia mwenziwe kilema; vile vile kama alivyofanya, naye atafanyiwa vivyo; 20 jeraha kwa jeraha, jicho kwa jicho, jino kwa jino; vile vile kama alivyomtia mtu kilema, naye atalipwa vivyo. 21 Na mtu amwuaye mnyama atalipa; na yeye atakayemwua binadamu atauawa. 22 Mtakuwa na sheria moja tu, kwa huyo aliye mgeni, na kwa mzalia; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 23 Musa akanena na wana wa Israeli, nao wakamtoa huyo aliyeapiza nje ya marago, wakamwua kwa kumpiga kwa mawe. Wana wa Israeli wakafanya kama Bwana alivyomwagiza Musa.

Mambo ya Walawi 25

1 Kisha Bwana akanena na Musa katika mlima wa Sinai, na kumwambia, 2 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Hapo mtakapoingia katika nchi niwapayo, ndipo hiyo nchi itashika Sabato kwa ajili ya Bwana. 3 Panda shamba lako miaka sita, na miaka sita lipelee shamba lako la mizabibu, na kuyachuma matunda yake; 4 lakini katika mwaka wa saba itakuwa ni Sabato ya kustarehe kabisa kwa ajili ya hiyo nchi, ni Sabato kwa Bwana; usipande shamba lako, wala usipelee shamba lako la mizabibu. 5 Hicho kimeacho chenyewe katika mavuno yako, usikivune, wala zabibu za mizabibu isiyopelewa usizitunde; utakuwa mwaka wa kustarehe kabisa kwa ajili ya hiyo nchi. 6 Na hiyo Sabato ya nchi itakuwa chakula kwenu; kwako wewe, na kwa mtumwa wako, na kwa mjakazi wako, na kwa mtumishi aliyeajiriwa, na kwa mgeni wako akaaye pamoja nawe; 7 na kwa hayawani wako, na kwa wanyama walio katika nchi yako; maongeo yote yatakuwa ni chakula chao. 8 Nawe utajihesabia Sabato saba za miaka, maana, miaka saba mara saba; zitakuwa ni siku za Sabato saba za miaka kwenu, maana miaka arobaini na kenda. 9 Ndipo utakapoipeleka pande zote hiyo baragumu yenye sauti kuu, siku ya kumi ya mwezi wa saba; katika siku hiyo ya upatanisho mtaipeleka baragumu katika nchi yenu yote. 10 Na mwaka wa hamsini mtautakasa, na kupiga mbiu ya kuachwa mahuru katika nchi yote kwa watu wote wanayokaa; itakuwa ni yubile kwenu, nanyi kila mtu atairudia milki yake mwenyewe, nanyi mtarejea kila mtu kwa jamaa yake. 11 Mwaka huo wa hamsini utakuwa ni yubile kwenu; msipande mbegu, wala msivune kitu hicho kimeacho chenyewe, wala msizitunde zabibu za mizabibu isiyopelewa. 12 Kwa kuwa ni yubile; utakuwa mwaka mtakatifu kwenu; mtakula maongeo yake yatokayo shambani. 13 Mwaka huo wa yubile mtairudia kila mtu milki yake. 14 Tena kama ukimwuzia jirani yako cho chote, au kununua cho chote mkononi mwa jirani yako, msidanganyane wenyewe kwa wenyewe; 15 kwa hesabu ya miaka iliyo baada ya yubile, ndivyo utakavyonunua kwa jirani yako, na kama hesabu ya miaka ya mavuno ndivyo atakavyokuuzia wewe. 16 Kama hesabu ya miaka ilivyo ni nyingi ndivyo utakavyoongeza bei yake, na kama hesabu ya miaka ilivyo ni chache ndivyo utakavyopunguza bei yake; kwani yeye akuuzia mavuno kama hesabu yake ilivyo. 17 Wala msidanganyane; lakini utamcha Mungu wako; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 18 Kwa sababu hii zitendeni amri zangu, mkazishike hukumu zangu, na kuzifanya; nanyi mtakaa katika hiyo nchi salama. 19 Nayo nchi itazaa matunda yake, nanyi mtakula na kushiba, na kuketi humo salama. 20 Na kama mkisema, Je! Mwaka wa saba tutakula nini? Angalieni hatutapanda mbegu, wala kukusanya maongeo yetu; 21 ndipo nitawaamria baraka yangu iwe juu yenu mwaka wa sita, nayo utazaa matunda hesabu ya miaka mitatu. 22 Na mwaka wa nane mtapanda mbegu, na kuyala yale matunda, akiba hiyo ya zamani, hata mwaka wa kenda, hata matunda yake yatakapoletwa ndani, mtakula hiyo akiba ya zamani. 23 Nayo nchi haitauzwa kabisa kabisa; kwani nchi ni yangu mimi; maana ninyi ni wageni na wasafiri wangu. 24 Nanyi mtatoa ukombozi kwa ajili ya nchi, katika nchi yote ya milki yenu. 25 Kwamba nduguyo amekuwa maskini, na kuuza sehemu ya milki yake, ndipo jamaa yake aliye karibu naye atakuja, naye ataikomboa ile aliyoiuza nduguye. 26 Na kama mtu hana atakayeikomboa, naye mwenyewe amepata mali na kujiona kuwa anayo ya kutosha kuikomboa; 27 ndipo na aihesabu hiyo miaka ya kuuzwa kwake, na kilichozidi kumrudishia huyo mtu aliyeinunua; naye atairejea milki yake. 28 Lakini asipoweza kujipatia mwenyewe, ndipo hiyo iliyouzwa itakaa mkononi mwake huyo aliyeinunua, hata mwaka wa yubile; na katika yubile itatoka, naye atairejea milki yake. 29 Tena kwamba mtu anauza nyumba ya kukaa, iliyo ndani ya mji wenye kuta, ndipo ana ruhusa kuikomboa katika mwaka mmoja mzima baada ya kuiuza; atakuwa na amri ya kuikomboa muda wa mwaka mzima. 30 Na kama haikukombolewa katika muda wa mwaka mzima, ndipo hiyo nyumba iliyo ndani ya mji wenye kuta itathibitishwa milele kuwa ya huyo aliyeinunua, katika vizazi vyake; nayo haitatoka katika yubile. 31 Lakini nyumba za vijiji, ambavyo havikuzingirwa na kuta, zitahesabiwa pamoja na mashamba ya nchi; nazo zina ruhusa ya kukombolewa, nazo zitatoka katika yubile. 32 Pamoja na hayo, miji ya Walawi, nyumba za miji ya milki yao, Walawi wana ruhusa ya kuzikomboa majira yo yote. 33 Tena kama mtu mmoja wa hao Walawi akikomboa, ndipo nyumba iliyouzwa, na mji wa milki yake, itatoka katika yubile; maana, hizo nyumba za miji ya Walawi ni milki yao kati ya wana wa Israeli. 34 Lakini konde la malisho ya miji yao lisiuzwe kwa kuwa ni milki yao ya daima. 35 Na ikiwa ndugu yako amekuwa maskini, na mkono wake umelegea kwako, ndipo utamsaidia, atakaa nawe kama mgeni, na msafiri. 36 Usitake riba kwake wala faida, bali mche Mungu wako, ili ndugu yako akae nawe. 37 Usimpe fedha yako upate riba, wala usimpe vyakula vyako kwa kujitakia faida. 38 Mimi ndimi Bwana, Mungu wako, niliyewatoa katika nchi ya Misri ili niwape nchi ya Kanaani, nipate kuwa Mungu wenu. 39 Tena kwamba nduguyo amekuwa maskini pamoja nawe, akajiuza kwako; usimtumikishe mfano wa mtumwa; 40 kwako wewe atakuwa mfano wa mtumishi aliyeajiriwa, au mfano wa msafiri; naye atatumika kwako hata mwaka wa yubile; 41 ndipo atakapotoka kwako aende zake, yeye na wanawe pamoja naye, naye atairejea jamaa yake mwenyewe, tena atairejea milki ya baba zake. 42 Kwa kuwa hao ni watumishi wangu, niliowaleta watoke nchi ya Misri; wasiuzwe mfano wa watumwa. 43 Usitawale juu yake kwa nguvu; ila umche Mungu wako. 44 Tena katika habari za watumwa wako na wajakazi wako, utakaokuwa nao; mataifa walio kando-kando yenu, katika hao mtanunua watumwa na wajakazi. 45 Tena katika wana wa wageni wakaao kati yenu mtajinunulia, na katika jamaa zao walio pamoja nanyi, waliowazaa katika nchi yenu; wao watakuwa milki yenu. 46 Nanyi mtawafanya kuwa urithi kwa watoto wenu baada yenu, wawe milki yao; siku zote mtatwaa watumwa wenu katika hao; lakini msitawale kwa nguvu juu ya ndugu zenu, hao wana wa Israeli, wenyewe kwa wenyewe. 47 Tena kama mgeni au mtu akaaye nawe akitajirika, na nduguyo amekuwa maskini karibu naye, akajiuza kwa huyo mgeni, au kwa huyo akaaye kwako, au kwa ukoo wa jamaa ya huyo mgeni; 48 baada ya kuuzwa aweza kukombolewa; mtu mmoja miongoni mwa ndugu zake ana ruhusa kumkomboa; 49 au mjomba wake, au mwana wa mjomba wake, ana ruhusa ya kumkomboa, au mtu awaye yote aliye karibu naye wa jamaa yake, ana ruhusa ya kumkomboa; au kwamba yeye mwenyewe amepata mali, ana ruhusa ya kujikomboa mwenyewe. 50 Naye atafanya hesabu na huyo aliyemnunua, tangu mwaka huo aliojiuza hata mwaka wa yubile; na ile bei ya kuuzwa kwake itakuwa kama hesabu ya hiyo miaka ilivyo; atakuwa pamoja naye kama majira ya mtumishi aliyeajiriwa yalivyo. 51 Kwamba ikali imesalia miaka mingi, kama hesabu yake ilivyo ndivyo atakavyolipa bei ya ukombozi wake, katika hiyo fedha ambayo alinunuliwa kwayo. 52 Tena kwamba imesalia miaka michache tu hata mwaka wa yubile, ndipo atafanya hesabu naye, kama hesabu ya miaka yake ilivyo, ndivyo atakavyolipa tena bei ya ukombozi wake. 53 Kama mtumishi aliyeajiriwa mwaka hata mwaka, ndivyo atakavyokuwa pamoja naye; asitawale juu yake kwa nguvu mbele ya macho yako. 54 Tena kwamba hakukombolewa kwa njia hizi mojawapo, ndipo atatoka katika mwaka wa yubile, yeye, na watoto wake pamoja naye. 55 Kwa kuwa wana wa Israeli ni watumishi; ni watumishi wangu niliowaleta watoke katika nchi ya Misri; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.

Mambo ya Walawi 26

1 Msifanye sanamu yo yote, wala msijisimamishie sanamu ya kuchonga, wala mnara, wala msiweke jiwe lo lote lililochorwa katika nchi yenu ili kulisujudia; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 2 Zishikeni Sabato zangu, na kupastahi patakatifu pangu; mimi ndimi Bwana. 3 Kama mkienda katika amri zangu, na kuyashika maagizo yangu, na kuyafanya; 4 ndipo nitazinyesha mvua zenu kwa nyakati zake, na nchi itazaa maongeo yake, na miti ya mashambani itazaa matunda yake. 5 Tena kupura nafaka kwenu kutaendelea hata wakati wa kuvuna zabibu, na kuvuna zabibu kutaendelea hata wakati wa kupanda mbegu; nanyi mtakula chakula chenu na kushiba, na kuketi katika nchi yenu salama. 6 Nami nitawapa amani katika nchi, tena mtalala wala hapana atakayewatia hofu; nami nitawakomesha wanyama wabaya katika nchi yenu, wala hautapita upanga katika nchi yenu. 7 Nanyi mtawafukuza adui zenu, nao wataanguka mbele zenu kwa upanga. 8 Na watu watano wa kwenu watawafukuza watu mia, na watu mia wa kwenu watawafukuza watu elfu kumi; na adui zenu wataanguka mbele yenu kwa upanga. 9 Nami nitawaelekezea uso wangu, na kuwapa uzazi mwingi, na kuwaongeza; nami nitalithibitisha agano langu pamoja nanyi. 10 Nanyi mtakula akiba ya zamani mliyoiweka siku nyingi, tena hayo ya zamani mtayatoa, ili myaweke yaliyo mapya. 11 Nami nitaiweka maskani yangu kati yenu; wala roho yangu haitawachukia. 12 Nami nitakwenda kati yenu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu. 13 Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, niliyewaleta mtoke katika nchi ya Misri, ili msiwe watumwa wao; nami nimeivunja miti ya kongwa lenu, nikawaendesha mwende sawasawa. 14 Lakini msiponisikiza, wala hamtaki kuyafanya maagizo hayo yote; 15 nanyi mkizikataa amri zangu, na roho yenu ikichukia hukumu zangu, hata ikawa hamtaki kuyafanya maagizo yangu yote, bali mwalivunja agano langu; 16 mimi nami nitawatenda jambo hili; nitaamrisha uje juu yenu utisho, hata kifua kikuu na homa, zitakazoharibu macho yenu, na kuidhoofisha roho; nanyi mtapanda mbegu yenu bure, kwa kuwa adui zenu wataila. 17 Nami nitauelekeza uso wangu kinyume chenu, nanyi mtapigwa mbele ya adui zenu; hao wawachukiao watatawala juu yenu; nanyi mtakimbia wakati ambao hapana awafukuzaye. 18 Tena ikiwa baada ya hayo hamtaki kunisikiza, ndipo nitawaadhibu zaidi mara saba kwa ajili ya dhambi zenu. 19 Nami nitakivunja kiburi cha uwezo wenu; nami nitazifanya mbingu zenu kuwa kama chuma, na nchi yenu kuwa kama shaba; 20 na nguvu zenu mtazitumia bure; kwa kuwa nchi yenu haitazaa mazao yake, wala miti ya nchi haitazaa matunda yake. 21 Nanyi ikiwa mwaenenda kinyume changu, wala hamtaki kunisikiza; nitaleta mapigo mara saba zaidi juu yenu, kama dhambi zenu zilivyo. 22 Nami nitaleta wanyama wakali kati yenu, ambao watawanyang'anya watoto wenu, na kuwaharibu wanyama wenu wa kufugwa, na kuwapunguza muwe wachache hesabu yenu; na njia zenu zitakuwa ni ukiwa. 23 Tena kama hamtaki kurejezwa upya kwangu mimi kwa mambo haya, bali mwaendelea kunishikia kinyume; ndipo mimi nami nitaendelea kuwashikia ninyi kinyume; 24 nami nitawapiga, naam mimi, mara saba kwa ajili ya dhambi zenu. 25 Nami nitaleta upanga juu yenu, utakaopatiliza kisasi cha hilo agano; nanyi mtakutanishwa ndani ya miji yenu; nami nitaleta tauni kati yenu; nanyi mtatiwa mkononi mwa adui. 26 Hapo nitakapovunja tegemeo lenu la mkate, wanawake kumi wataoka mikate yenu katika tanuu moja, nao watawapa mikate yenu tena kwa kupima kwa mizani; nanyi mtakula, lakini hamtashiba. 27 Tena ikiwa baada ya hayo yote hamtaki kunisikiza, bali mwaenenda kwa kunishikia kinyume; 28 ndipo nami nitakwenda kwa kuwashikia ninyi kinyume katika ghadhabu yangu; nami nitawaadhibu mara saba kwa dhambi zenu. 29 Nanyi mtakula nyama ya miili ya wana wenu, na nyama ya miili ya binti zenu mtaila. 30 Nami nitapaharibu mahali penu palipoinuka, na kuziangusha sanamu zenu za jua, nami nitaitupa mizoga yenu juu ya mizoga ya sanamu zenu; na roho yangu itawachukia. 31 Nami nitaifanya miji yenu iwe maganjo, na mahali penu patakatifu nitapatia ukiwa; wala sitasikia harufu ya manukato yenu yapendezayo. 32 Nami nitaitia hiyo nchi ukiwa; na adui zenu watakaokaa huko wataistaajabia. 33 Nanyi nitawatapanya-tapanya katika mataifa, nami nitaufuta upanga nyuma yenu; na nchi yenu itakuwa ni ukiwa, na miji yenu maganjo. 34 Hapo ndipo nchi itakapozifurahia Sabato zake, wakati itakapokuwa hali ya ukiwa, nanyi mtakapokuwa katika nchi ya adui zenu; ndipo nchi itakapopumzika, na kuzifurahia Sabato zake. 35 Wakati wote itakapokuwa na ukiwa, itapumzika; ni hayo mapumziko ambayo haikuwa nayo katika Sabato zenu, hapo mlipokaa katika nchi hiyo. 36 Tena hao wa kwenu watakaobaki, nitawatilia woga mioyoni mwao, katika hizo nchi za adui zao; na sauti ya jani lililopeperushwa itawakimbiza; nao watakimbia, kama mtu akimbiavyo upanga; nao wataanguka hapo ambapo hapana afukuzaye. 37 Nao wataangukiana wenyewe kwa wenyewe, kama mbele ya upanga, hapo ambapo hapana afukuzaye; wala hamtakuwa na nguvu za kusimama mbele ya adui zenu. 38 Nanyi mtaangamia kati ya mataifa, na nchi ya adui zenu itawameza. 39 Na watu wa kwenu watakaobaki watafifia kwa ajili ya uovu wao, katika hizo nchi za adui zenu; tena watafifia kwa ajili ya uovu wa baba zao, pamoja nao. 40 Nao wataukiri uovu wao, na uovu wa baba zao, katika maasi yao waliyoasi juu yangu, tena ya kuwa kwa sababu wameendelea kunishikia kinyume, 41 mimi nami nimeendelea kuwashikia kinyume wao, na kuwatia katika nchi ya adui zao; lakini hapo, kama mioyo yao isiyokuwa tohara ikinyenyekea, nao wakubali adhabu ya uovu wao; 42 ndipo nitakapokumbuka agano langu pamoja na Yakobo, tena agano langu na Isaka, tena agano langu na Ibrahimu nitalikumbuka; nami nitaikumbuka nchi hiyo. 43 Nchi nayo itaachwa na wao, nayo itazifurahia Sabato zake, itakapokuwa ukiwa pasipokuwa na wao; nao wataikubali adhabu ya uovu wao; kwa sababu, naam, ni kwa sababu wamezikataa hukumu zangu, na roho zao zimezichukia amri zangu. 44 Lakini pamoja na hayo yote, watakapokuwa katika nchi ya adui zao, mimi, sitawatupa, wala sitawachukia, niwaangamize kabisa, na kulivunja agano langu pamoja nao; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wao; 45 lakini kwa ajili yao nitalikumbuka agano la baba zao, niliowaleta watoke katika nchi ya Misri mbele ya macho ya mataifa, ili kwamba niwe Mungu wao; mimi ndimi Bwana. 46 Hizi ni amri na hukumu na sheria, Bwana alizozifanya kati ya yeye na hao wana wa Israeli katika huo mlima wa Sinai kwa mkono wa Musa.

Mambo ya Walawi 27

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Hapo mtu atakapoondoa nadhiri, hizo nafsi za watu zitakuwa kwa Bwana, kama utakavyowahesabia wewe. 3 Na hesabu yako itakuwa kwa mtu mume, tokea aliye na umri wa miaka ishirini hata umri wa miaka sitini, hesabu yako itakuwa shekeli hamsini za fedha, kwa shekeli ya mahali patakatifu. 4 Kama ni mwanamke, hesabu yako itakuwa shekeli thelathini. 5 Tena akiwa mwenye umri wa miaka mitano hata umri wa miaka ishirini, ndipo hesabu yako itakuwa shekeli ishirini kwa mwanamume, na shekeli kumi kwa mwanamke. 6 Tena akiwa mwenye umri wa mwezi mmoja hata umri wa miaka mitano, ndipo hesabu yako itakuwa shekeli tano za fedha kwa mwanamume, na hesabu yako itakuwa shekeli tatu za fedha kwa mwanamke. 7 Tena akiwa mwenye umri wa miaka sitini na kuzidi; kama ni mwanamume, hesabu yako itakuwa shekeli kumi na tano, na kwa mwanamke shekeli kumi. 8 Lakini kwamba ni maskini zaidi ya kuhesabu kwako, ndipo atawekwa mbele ya kuhani, na huyo kuhani atamtia kima; kama uwezo wake huyo aliyeweka nadhiri ulivyo, ndivyo kuhani atakavyomtia kima. 9 Tena kama ni mnyama wa namna ambayo watu husongeza kuwa sadaka kwa Bwana, kila mmoja katika wanyama hao atakayetolewa kwa Bwana, na mtu ye yote, atakuwa ni mtakatifu. 10 Yeye hatamgeuza, wala kumbadili mwema kwa mbaya, au mbaya kwa mwema; kwamba atabadili mnyama kwa mnyama ye yote, ndipo mnyama huyo na yule waliobadiliwa wote wawili watakuwa watakatifu. 11 Na kama ni mnyama ye yote asiye safi, wa namna ambayo hawamsongezi kwa Bwana, basi atamweka huyo mnyama mbele ya kuhani; 12 na kuhani atamtia kima, akiwa mwema akiwa mbaya; kama wewe kuhani utakavyomtia kima, ndivyo itakavyokuwa. 13 Lakini kwamba ataka kumkomboa kweli, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano juu ya hesabu yako. 14 Na mtu atakapoiweka nyumba yake iwe wakfu kwa Bwana ndipo kuhani ataihesabu kima chake hiyo nyumba, ikiwa njema ikiwa mbaya; kama kuhani atakavyoihesabu kima chake ndivyo itakavyokuwa. 15 Tena mtu huyo aliyeweka nyumba yake iwe wakfu kama akitaka kuikomboa, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano ya hiyo fedha ya hesabu yako, nayo itakuwa mali yake. 16 Tena kama mtu akiweka wakfu kwa Bwana sehemu ya shamba la milki yake, ndipo hesabu yako itakuwa kama kule kupanda kwake kulivyo; kupanda kwake homeri moja ya mbegu ya shayiri, kutahesabiwa kuwa ni shekeli hamsini za fedha. 17 Kwamba anaweka shamba lake liwe wakfu tangu mwaka wa yubile, litasimama vivyo kama hesabu yako ilivyo. 18 Lakini akiliweka shamba lake wakfu baada ya yubile, ndipo kuhani atamhesabia hiyo fedha kama hesabu ya miaka iliyobaki hata mwaka wa yubile, na kuhesabiwa kwako kutapunguzwa. 19 Na kama yeye aliyeliweka shamba wakfu akitaka kulikomboa kweli, ndipo atakapoongeza sehemu ya tano ya hiyo fedha ya hesabu yako, nalo litathibitishwa kwake. 20 Lakini asipotaka kulikomboa shamba, au kama amemwuzia mtu mwingine hilo shamba, halitakombolewa tena kabisa; 21 ila hilo shamba litakuwa takatifu kwa Bwana litakapotoka katika yubile, kama ni shamba lililowekwa wakfu; litakuwa mali ya kuhani. 22 Tena kama akiweka wakfu kwa Bwana shamba ambalo amelinunua, ambalo si shamba la milki yake; 23 ndipo kuhani atamhesabia kima cha kuhesabu kwako hata mwaka wa yubile: naye atatoa siku hiyo kama hesabu yako, kuwa ni kitu kitakatifu kwa Bwana. 24 Mwaka wa yubile shamba hilo litarejea kwake huyo ambaye lilinunuliwa kwake, yaani, huyo ambaye nchi hiyo ni milki yake. 25 Na hesabu zako zote zitaandamana shekeli ya mahali patakatifu; gera ishirini zitakuwa shekeli moja. 26 Mzaliwa wa kwanza tu katika wanyama, aliyewekwa kuwa mzaliwa wa kwanza kwa Bwana, mtu awaye yote hatamweka kuwa mtakatifu; kama ni ng'ombe, kama ni kondoo, huyo ni wa Bwana. 27 Na kama ni wa mnyama asiye safi, ndipo atamkomboa kama hesabu yako ilivyo, naye ataongeza sehemu ya tano ya bei yake; au asipokombolewa, ndipo atauzwa kama hesabu yako ilivyo. 28 Pamoja na hayo, hakitauzwa wala kukombolewa kitu cho chote kilichowekwa wakfu, ambacho mtu amekiweka wakfu kwa Bwana, katika vitu vyote alivyo navyo, kama ni mtu, au mnyama, au kama ni shamba la milki yake; kila kitu kilichowekwa wakfu ni kitakatifu sana kwa Bwana. 29 Kila aliyewekwa wakfu, aliyewekwa wakfu na binadamu, hatakombolewa; sharti atauawa. 30 Tena zaka yote ya nchi, kama ni mbegu ya nchi, au kama ni matunda ya nchi, ni ya Bwana; ni takatifu kwa Bwana. 31 Na kama mtu akitaka kukomboa cho chote cha zaka yake, ataongeza sehemu yake ya tano juu yake. 32 Tena zaka yote ya ng'ombe, au ya kondoo, kila apitaye chini ya fimbo; sehemu ya kumi watakuwa ni watakatifu kwa Bwana. 33 Hataangalia kwamba ni mwema au kwamba ni mbaya, wala hatambadili; na kama akimbadili na yo yote, ndipo wote wawili, huyo na huyo waliobadiliwa watakuwa ni watakatifu; hatakombolewa. 34 Haya ndiyo maagizo, Bwana aliyomwagiza Musa kwa ajili ya wana wa Israeli katika mlima wa Sinai.

Hesabu 1

1 Bwana akanena na Musa katika bara ya Sinai, hemani mwa kukutania, siku ya kwanza ya mwezi wa pili, katika mwaka wa pili baada ya kutoka kwao nchi ya Misri, akamwambia, 2 Fanyeni hesabu ya mkutano wote wa wana wa Israeli, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina ilivyo, kila mtu mume kichwa kwa kichwa; 3 tangu mwenye miaka ishirini umri wake, na zaidi, wote wawezao kutoka kwenenda vitani katika Israeli; wewe na Haruni mtawahesabu kwa kuandama majeshi yao. 4 Tena mtu mume mmoja wa kila kabila atakuwa pamoja nanyi; kila mmoja aliye kichwa cha nyumba ya baba zake. 5 Na majina ya hao waume watakaosimama pamoja nanyi ni haya; Wa Reubeni; Elisuri mwana wa Shedeuri. 6 Wa Simeoni; Shelumieli mwana wa Suri-shadai. 7 Wa Yuda; Nashoni mwana wa Aminadabu. 8 Wa Isakari; Nethaneli mwana wa Suari. 9 Wa Zabuloni; Eliabu mwana wa Heloni. 10 Katika wana wa Yusufu; wa Efraimu, Elishama mwana wa Amihudi; na wa Manase; Gamalieli mwana wa Pedasuri. 11 Wa Benyamini Abidani mwana wa Gideoni. 12 Wa Dani; Ahiezeri mwana wa Amishadai. 13 Wa Asheri; Pagieli mwana wa Okirani. 14 Wa Gadi; Eliasafu mwana wa Deueli. 15 Wa Naftali; Ahira mwana wa Enani. 16 Hao ndio walioitwa wa mkutano, wakuu wa kabila za baba zao; nao ndio vichwa vya wale maelfu ya Israeli. 17 Basi Musa na Haruni wakawatwaa hao watu waume waliotajwa majina yao; 18 nao waliukutanisha mkutano mzima, siku ya kwanza ya mwezi wa pili, nao wakaonyesha ukoo wa vizazi vyao kwa kuandama jamaa zao, kwa nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, kichwa kwa kichwa. 19 Kama Bwana alivyomwagiza Musa, ndivyo alivyowahesabu huko katika bara ya Sinai. 20 Na wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, kichwa kwa kichwa, kila mtu mume tangu umri wa miaka ishirini na zaidi wote walioweza kwenda vitani; 21 wale waliohesabiwa katika kabila ya Reubeni, walikuwa watu arobaini na sita elfu na mia tano (46,500). 22 Katika wana wa Simeoni, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, wale waliohesabiwa kama hesabu ya majina, kichwa kwa kichwa, kila mume tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 23 wale waliohesabiwa katika kabila ya Simeoni, walikuwa watu hamsini na kenda elfu na mia tatu (59,300). 24 Katika wana wa Gadi, kwa kuandama vizazi vyao, jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 25 wale waliohesabiwa katika kabila ya Gadi, walikuwa watu arobaini na tano elfu na mia sita na hamsini (45,650). 26 Katika wana wa Yuda, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 27 wale waliohesabiwa katika kabila ya Yuda, walikuwa watu sabini na nne elfu na mia sita (74,600). 28 Katika wana wa Isakari, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kwa hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 29 wale waliohesabiwa katika kabila ya Isakari, walikuwa watu hamsini na nne elfu na mia nne (54,400). 30 Katika wana wa Zabuloni, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 31 wale waliohesabiwa katika kabila ya Zabuloni, walikuwa watu hamsini na saba elfu na mia nne (57,400). 32 Katika wana wa Yusufu, maana katika wana wa Efraimu, vizazi vyao kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani, 33 wale waliohesabiwa katika kabila ya Efraimu, walikuwa watu arobaini elfu na mia tano (40,500). 34 Katika wana wa Manase, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 35 wale waliohesabiwa katika kabila ya Manase, walikuwa watu thelathini na mbili elfu na mia mbili (32,200). 36 Katika wana wa Benyamini, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 37 wale waliohesabiwa katika kabila ya Benyamini, walikuwa watu thelathini na tano elfu na mia nne (35,400). 38 Katika wana wa Dani, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 39 wale waliohesabiwa katika kabila ya Dani, walikuwa watu sitini na mbili elfu na mia saba (62,700). 40 Katika wana wa Asheri, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 41 wale waliohesabiwa katika kabila ya Asheri, walikuwa watu arobaini na moja elfu na mia tano (41,500). 42 Katika wana wa Naftali, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani; 43 wale waliohesabiwa katika kabila ya Naftali, walikuwa watu hamsini na tatu elfu na mia nne (53,400). 44 Hao ndio waliohesabiwa, ambao Musa na Haruni na wale wakuu wa Israeli watu kumi na wawili waliwahesabu; walikuwa kila mmoja kwa ajili ya nyumba ya baba zake. 45 Basi hao wote waliohesabiwa katika wana wa israeli kwa kuandama nyumba za baba zao tangu umri wa miaka ishirini na zaidi; wote walioweza kwenda vitani katika Israeli; 46 hao wote waliohesabiwa walikuwa ni watu waume mia sita na tatu elfu na mia tano na hamsini (603,550). 47 Lakini Walawi kwa kuiandama kabila ya baba zao hawakuhesabiwa katika watu hao. 48 Kwa kuwa Bwana alinena na Musa, na kumwambia, 49 Hiyo kabila ya Lawi tu usiihesabu, wala usiitie hesabu yao katika wana wa Israeli; 50 lakini uwaweke Walawi wawe juu ya maskani ya ushahidi, na juu ya vyombo vyake vyote, na juu ya vitu vyake vyote; wao wataichukua hiyo maskani, na vyombo vyake vyote; nao wataitumikia, na kupanga hema zao kwa kuizunguka maskani pande zote. 51 Tena hapo maskani itakapokwenda mbele, Walawi wataishusha; tena hapo maskani itakaposimamishwa, Walawi wataisimamisha; na mgeni atakayekaribia atauawa. 52 Na wana wa Israeli watazipanga hema zao, kila mtu katika marago yake mwenyewe, kila mtu hapo ilipo beramu yake mwenyewe, kama majeshi yao yalivyo. 53 Lakini Walawi watapanga hema zao kuizunguka maskani ya ushahidi pande zote, ili zisiwe hasira juu ya mkutano wa wana wa Israeli; kisha Walawi wataulinda ulinzi wa hiyo maskani ya ushahidi. 54 Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli; kama yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyofanya.

Hesabu 2

1 Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 2 Wana wa Israeli watapanga kila mtu penye beramu yake mwenyewe, na alama za nyumba za baba zao; kuikabili hema ya kukutania ndiko watakakopanga kwa kuizunguka pande zote. 3 Na hao watakaopanga upande wa mashariki, kwa kuelekea maawio ya jua, ndio wale wa beramu ya marago ya Yuda, kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Yuda atakuwa Nashoni mwana wa Aminadabu. 4 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa sabini na nne elfu na mia sita. 5 Na hao watakaopanga karibu naye ni kabila ya Isakari; na mkuu wa wana wa Isakari atakuwa Nethaneli mwana wa Suari; 6 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na nne elfu na mia nne; 7 na kabila ya Zabuloni; na mkuu wa wana wa Zabuloni atakuwa Eliabu mwana wa Heloni; 8 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na saba elfu na mia nne. 9 Hao wote waliohesabiwa katika marago ya Yuda walikuwa mia na themanini na sita elfu na mia nne, kwa majeshi yao. Hao ndio watakaosafiri mbele. 10 Upande wa kusini kutakuwa na beramu ya marago ya Reubeni kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Reubeni atakuwa Elisuri mwana wa Shedeuri. 11 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa arobaini na sita elfu na mia tano. 12 Na hao watakaopanga karibu naye ni kabila ya Simeoni; na mkuu wa wana wa Simeoni atakuwa Shelumieli mwana wa Suri-shadai; 13 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na kenda elfu na mia tatu; 14 na kabila ya Gadi; na mkuu wa wana wa Gadi atakuwa Eliasafu mwana wa Deueli; 15 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa arobaini na tano elfu na mia sita na hamsini. 16 Wote waliohesabiwa katika marago ya Reubeni walikuwa mia na hamsini na moja elfu na mia nne na hamsini, kwa majeshi yao. Nao ndio watakaosafiri mahali pa pili. 17 Ndipo hema ya kukutania itasafiri, pamoja na marago ya Walawi katikati ya marago yote; kama wapangavyo marago, watasafiri vivyo, kila mtu mahali pake, penye beramu zao. 18 Upande wa magharibi kutakuwa na beramu ya marago ya Efraimu kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Efraimu atakuwa Elishama mwana wa Amihudi. 19 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao walikuwa arobaini elfu na mia tano. 20 Na karibu naye itakuwa kabila ya Manase; na mkuu wa wana wa Manase atakuwa Gamalieli mwana wa Pedasuri; 21 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa thelathini na mbili elfu na mia mbili; 22 tena kabila ya Benyamini; na mkuu wa wana wa Benyamini atakuwa Abidani mwana wa Gideoni; 23 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa thelathini na tano elfu na mia nne. 24 Wote waliohesabiwa katika marago ya Efraimu walikuwa mia na nane elfu na mia moja, kwa majeshi yao. Nao ndio watakaosafiri katika mahali pa tatu. 25 Upande wa kaskazini kutakuwa na beramu ya marago ya Dani kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Dani atakuwa Ahiezeri mwana wa Amishadai. 26 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa sitini na mbili elfu na mia saba. 27 Na hao watakaopanga karibu naye ni kabila ya Asheri; na mkuu wa wana wa Asheri atakuwa Pagieli mwana wa Okrani; 28 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa arobaini na moja elfu na mia tano; 29 kisha kabila ya Naftali; na mkuu wa wana wa Naftali atakuwa Ahira mwana wa Enani; 30 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na tatu elfu na mia nne. 31 Wote waliohesabiwa katika marago ya Dani walikuwa mia na hamsini na saba elfu na mia sita. Hao ndio watakaosafiri mwisho kwa kuandama beramu zao. 32 Hao ndio waliohesabiwa katika wana wa Israeli kwa nyumba za baba zao; wote waliohesabiwa katika marago kwa majeshi yao, walikuwa mia sita na tatu elfu na mia tano na hamsini. 33 Lakini Walawi hawakuhesabiwa katika wana wa Israeli; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 34 Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli; kama yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyopanga penye beramu zao, na ndivyo walivyosafiri, kila mtu kwa jamaa zao, kwa nyumba za baba zao.

Hesabu 3

1 Basi vizazi vya Haruni na Musa, siku hiyo Bwana aliyosema na Musa katika mlima wa Sinai, ni hivi. 2 Tena majina ya hao wana wa Haruni ni haya; Nadabu mzaliwa wa kwanza, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari. 3 Hayo ndiyo majina ya wana wa Haruni, hao makuhani waliotiwa mafuta, ambao aliwaweka wakfu ili wafanye kazi ya ukuhani. 4 Kisha Nadabu na Abihu walikufa mbele za Bwana, waliposongeza moto wa kigeni mbele za Bwana, katika bara ya Sinai, nao walikuwa hawana wana; na Eleazari na Ithamari wakafanya kazi ya ukuhani mbele ya uso wa Haruni baba yao. 5 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 6 Ilete karibu kabila ya Lawi, ukawaweke mbele ya Haruni kuhani, ili wapate kumtumikia. 7 Nao wataulinda ulinzi wake, na ulinzi wa mkutano wote mbele ya hema ya kukutania, ili watumike utumishi wa maskani. 8 Nao watavitunza vyombo vyote vya hema ya kukutania, na kulinda ulinzi wa wana wa Israeli, ili watumike utumishi wa maskani. 9 Nawe utawapa Haruni na wanawe hao Walawi wawe nao; amepewa watu hao kabisa kwa ajili ya wana wa Israeli. 10 Nawe utawaweka Haruni na wanawe, nao wataushika ukuhani wao, na mgeni atakayekaribia atauawa. 11 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 12 Mimi, tazama, nimewatwaa Walawi na kuwatoa kati ya wana wa Israeli badala ya wazaliwa wa kwanza wote wafunguao tumbo katika wana wa Israeli; na hao Walawi watakuwa wangu; 13 kwa kuwa hao wazaliwa wa kwanza wote ni wangu; katika siku ile niliyowapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri nikajiwekea wakfu wazaliwa wa kwanza wote wa Israeli, wa wanadamu na wa wanyama; watakuwa wangu; mimi ndimi Bwana. 14 Kisha Bwana akanena na Musa huko katika bara ya Sinai, na kumwambia, 15 Uwahesabu wana wa Lawi kwa kuandama nyumba za baba zao na jamaa zao; kila mtu mume tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi utawahesabu. 16 Basi Musa akawahesabu kama neno la Bwana kama alivyoagizwa. 17 Na wana wa Lawi walikuwa ni hawa kwa majina yao; Gershoni, na Kohathi, na Merari. 18 Na majina ya wana wa Gershoni kwa jamaa zao ni Libni na Shimei. 19 Na wana wa Kohathi kwa jamaa zao ni Amramu, na Ishari, na Hebroni, na Uzieli. 20 Na wana wa Merari kwa jamaa zao ni Mahli, na Mushi. Hizi ndizo jamaa za Walawi kwa nyumba za baba zao. 21 Katika Gershoni walikuwa jamaa ya Walibni, na jamaa ya Washimei, hawa ndio jamaa za Wagershoni. 22 Hao waliohesabiwa kwao, kama hesabu ya waume wote, tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi, hao waliohesabiwa kwao walikuwa saba elfu na mia tano. 23 Jamaa za Wagershoni watapanga rago nyuma ya maskani, upande wa magharibi. 24 Na mkuu wa nyumba ya baba zao Wagershoni atakuwa Eliasafu mwana wa Laeli. 25 Na ulinzi wa Wagershoni katika hema ya kukutania ni hiyo maskani, na Hema, na kifuniko chake, na pazia la mlango wa hema ya kukutania, 26 na kuta za nguo za ua, na sitara ya mlango wa ua, iliyo karibu na maskani, na karibu na madhabahu pande zote, na kamba zake zitumiwazo kwa matumizi yake yote. 27 Na katika Kohathi ni jamaa ya Waamrami, na jamaa ya Waishari, na jamaa ya Wahebroni, na jamaa ya hao Wauzieli; hizo ni jamaa za Wakohathi. 28 Kama hesabu ya waume wote, tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi, walikuwa elfu nane na mia sita, wenye kuulinda ulinzi wa mahali patakatifu. 29 Jamaa za wana wa Kohathi watapanga rago upande wa kusini wa maskani. 30 Na mkuu wa nyumba ya baba za jamaa za Wakohathi atakuwa Elisafani mwana wa Uzieli. 31 Na vitu watakavyovitunza ni hilo sanduku, na meza, na kinara cha taa, na madhabahu, na vile vyombo vya mahali patakatifu wavitumiavyo katika kutumika kwao, na pazia, na utumishi wake wote. 32 Na Eleazari mwana wa Haruni kuhani atakuwa mkuu wa hao wakuu wa Walawi, naye atawasimamia hao walindao ulinzi wa mahali patakatifu. 33 Katika Merari ni jamaa ya hao Wamahli, na jamaa ya Wamushi; hizo ni jamaa za Merari. 34 Na hao waliohesabiwa kwao, kama hesabu ya waume wote, tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi, walikuwa sita elfu na mia mbili. 35 Na mkuu wa nyumba ya baba za jamaa za Merari alikuwa Surieli mwana wa Abihaili; hao watapanga rago upande wa maskani, wa kaskazini. 36 Na usimamizi walioamriwa wana wa Merari ulikuwa ni kutunza mbao za maskani, na mataruma yake, na nguzo zake, na matako yake, na vyombo vyake vyote, na utumishi wake wote; 37 na nguzo za ua zilizouzunguka, na matako yake, na vigingi vyake, na kamba zake. 38 Na hao watakaopanga mbele ya maskani upande wa mashariki, mbele ya hema ya kukutania upande wa kuelekea maawio ya jua, watakuwa hawa, Musa na Haruni na wanawe, wenye kulinda ulinzi wa mahali patakatifu, yaani, huo ulinzi wa wana wa Israeli; na mgeni atakayekaribia atauawa. 39 Hao wote waliohesabiwa katika Walawi, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana, kwa jamaa zao, waume wote tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi, walikuwa ishirini na mbili elfu. 40 Kisha Bwana akamwambia Musa, Uwahesabu waume wote wazaliwa wa kwanza katika wana wa Israeli tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi uyahesabu majina yao. 41 Nawe utawatwaa Walawi kwa ajili yangu mimi (Mimi ndimi Bwana) badala ya hao wazaliwa wa kwanza wote katika wana wa Israeli; na wanyama wa Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza wa wanyama wa wana wa Israeli. 42 Musa akahesabu, kama Bwana alivyomwagiza, wazaliwa wa kwanza wote katika wana wa Israeli. 43 Wazaliwa wa kwanza wote walio waume kwa hesabu ya majina, tangu umri wa mwezi mmoja na zaidi, katika hao waliohesabiwa kwao, walikuwa ishirini na mbili elfu na mia mbili na sabini na watatu. 44 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 45 Uwatwae Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza katika wana wa Israeli, na wanyama wa Walawi badala ya wanyama wao; na hao Walawi watakuwa wangu mimi; mimi ndimi Bwana. 46 Tena kwa kuwakomboa hao watu mia mbili na sabini na watatu, wa hao wazaliwa wa kwanza wa Israeli, ambao wamezidi ile hesabu ya Walawi, 47 utatwaa shekeli tano kwa kichwa cha kila mtu kwa hiyo shekeli ya mahali patakatifu (shekeli ni gera ishirini); 48 na hizo fedha ambazo waliosalia wamekombolewa kwazo utampa Haruni na wanawe. 49 Basi Musa akawatoza fedha za ukombozi, hao waliozidi hesabu ya wale waliokombolewa na Walawi; 50 akatwaa hizo fedha kwa wazaliwa wa kwanza wa wana wa Israeli; shekeli elfu moja na mia tatu na sitini na tano kwa shekeli ya mahali patakatifu; 51 kisha hizo fedha za ukombozi Musa akampa Haruni na wanawe, kama neno la Bwana, kama Bwana alivyomwagiza Musa.

Hesabu 4

1 Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 2 Katika wana wa Lawi uitenge hesabu ya wana wa Kohathi, kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao, 3 tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi hata umri wa miaka hamsini, wote waingiao katika utumishi huo, ili kufanya kazi ya hema ya kukutania. 4 Huu ndio utumishi wa wana wa Kohathi katika hema ya kukutania, katika vile vyombo vitakatifu sana; 5 hapo watakapong'oa safari, Haruni ataingia ndani, na wanawe, nao watalishusha pazia la sitara, na kulifunika sanduku la ushahidi kwa hilo pazia; 6 kisha atatia juu yake ngozi za pomboo za kulifunikia, na kutandika juu yake nguo ya rangi ya samawi tupu, kisha watatia hiyo miti yake. 7 Tena juu ya meza ya mikate ya wonyesho watatandika nguo ya rangi ya samawi, na kuweka juu yake sahani, na miiko, na mabakuli, na vikombe vya kumiminia; na hiyo mikate ya daima itakuwa juu yake; 8 nao watatandika juu yake nguo ya rangi nyekundu, na kuifunika kwa ngozi za pomboo za kuifunikia, na kuitia ile miti yake. 9 Kisha watatwaa nguo ya rangi ya samawi, na kukifunika kinara cha taa ya nuru, na taa zake, na makasi yake, na sahani zake za kutilia makaa, na vyombo vyake vyote vya mafuta, watumiavyo kwa kazi yake; 10 nao watakitia, na vyombo vyake vyote, ndani ya ngozi ya pomboo, na kukitia juu ya miti ya kukichukulia 11 Tena watatandika nguo ya rangi ya samawi juu ya madhabahu ya dhahabu, na kuifunika kwa ngozi za pomboo, na kuitia ile miti yake; 12 kisha watavitwaa vile vyombo vyote vya utumishi wavitumiavyo katika mahali patakatifu, na kuvitia katika nguo ya rangi ya samawi, na kuvifunika kwa ngozi za pomboo, na kuvitia juu ya miti ya kuvichukulia. 13 Nao watayaondoa hayo majivu madhabahuni; na kutandika nguo ya rangi ya zambarau juu yake; 14 nao wataweka vyombo vyake vyote juu yake ambavyo wavitumia katika madhabahu, vyetezo, na nyuma, na miiko, na mabakuli, vyombo vyote vya hiyo madhabahu; nao watatandika juu yake ngozi za pomboo, na kutia miti yake mahali pake. 15 Na Haruni na wanawe watakapokwisha kupafunika mahali patakatifu, na vyombo vyote vya mahali patakatifu, hapo watakapong'oa kambi; baadaye, wana wa Kohathi watakuja kuvichukua; lakini wasiviguse vile vitu vitakatifu, wasife. Vyombo vile ni mzigo wa wana wa Kohathi katika hema ya kukutania. 16 Na ulinzi wake Eleazari mwana wa Haruni kuhani utakuwa ni kuyaangalia mafuta kwa nuru, na uvumba mzuri, na sadaka ya unga ya daima, na mafuta ya kupaka, tena ulinzi wa hiyo maskani yote, na wa vitu vyote vilivyo ndani yake, mahali patakatifu, na vyombo vyake. 17 Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 18 Msiitenge kabisa kabila ya jamaa za Wakohathi katika hao Walawi; 19 lakini wafanyieni neno hili, ili kwamba wawe hai, wasife, hapo watakapovikaribia vile vitu vilivyo vitakatifu sana; Haruni na wanawe wataingia ndani, na kuwawekea kila mtu utumishi wake, na kila mtu mzigo wake; 20 lakini wasiingie wao kupaona mahali pale patakatifu, hata kwa dakika moja, ili wasife. 21 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 22 Fanya jumla ya wana wa Gershoni nao, kwa nyumba za baba zao, na jamaa zao; 23 tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini utawahesabu; wote watakaoingia kutumika, ili kufanya kazi katika hema ya kukutania. 24 Huu ni utumishi wa jamaa za Wagershoni, katika kutumika na katika kuchukua mizigo; 25 wao watayachukua mapazia ya maskani, na hema ya kukutania, hizo nguo za kufunikia, na zile ngozi za pomboo za kufunikia zilizo juu yake, na pazia la mlango wa hema ya kukutania; 26 na kuta za nguo za ua, na sitara ya ile nafasi ya kuingilia ya lango la ua, ulio karibu na maskani na madhabahu, kuzunguka pande zote, na kamba zake, na vyombo vyote vya utumishi wao, na yote yatakayotendeka kwavyo, watatumika katika hayo. 27 Utumishi wote wa wana wa Wagershoni, katika mzigo wao wote, na utumishi wao wote, utakuwa kwa amri ya Haruni na wanawe; nanyi mtawaagizia mzigo wao wote kuulinda. 28 Huu ni utumishi wa jamaa za wana wa Wagershoni katika hema kukutania; na ulinzi utakuwa chini ya mkono wa Ithamari mwana wa Haruni kuhani. 29 Katika habari ya wana wa Merari, utawahesabu kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao; 30 tangu aliyepata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, utawahesabu, kila atakayeingia katika huo utumishi, ili kufanya kazi ya hema ya kukutania. 31 Na mausia ya mzigo wao ni haya, kwa utumishi wao wote katika hema ya kukutania; mbao za maskani, na mataruma yake, na nguzo zake, na matako yake; 32 na viguzo vya ua vya kuuzunguka pande zote, na matako yake, na vigingi vyake, na kamba zake, na vyombo vyake vyote, pamoja na utumishi wake wote; nanyi mtawaagizia kila mtu kwa jina lake vile vyombo vya mzigo wao watakaoulinda. 33 Huu ni utumishi wa jamaa za wana wa Merari, kwa utumishi wao wote, katika hema ya kukutania, chini ya mkono wa Ithamari mwana wa Haruni kuhani. 34 Basi Musa na Haruni na hao wakuu wa mkutano wakawahesabu wana wa Kohathi kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao, 35 tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila mtu aliyeingia katika utumishi kwa kazi katika hema ya kukutania, 36 na waliohesabiwa kwao kwa jamaa zao, walikuwa elfu mbili na mia saba hamsini. 37 Hao ndio waliohesabiwa katika jamaa za Wakohathi, wote waliotumika katika hema ya kukutania, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana kwa mkono wa Musa. 38 Na hao waliohesabiwa katika wana wa Gershoni, kwa jamaa zao na nyumba zao baba zao, 39 tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila mtu aliyeingia katika utumishi, kwa kazi katika hema ya kukutania, 40 hata wale waliohesabiwa kwao, kwa jamaa zao na nyumba za baba zao, walikuwa elfu mbili na mia sita na thelathini. 41 Hao ndio waliohesabiwa katika jamaa za wana wa Gershoni, wote waliotumika katika hema ya kukutania, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana. 42 Na hao waliohesabiwa katika jamaa za wana wa Merari, kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao, 43 tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila mtu aliyeingia katika utumishi kwa kazi katika hema ya kukutania, 44 wale waliohesabiwa kwao, kwa jamaa zao, walikuwa elfu tatu na mia mbili. 45 Hao ndio waliohesabiwa katika jamaa za wana wa Merari, ambao Musa na; Haruni waliwahesabu kwa amri ya Bwana, kwa mkono wa Musa. 46 Wote waliohesabiwa katika Walawi, ambao Musa na Haruni na hao wakuu wa Israeli waliwahesabu, kwa jamaa zao, na nyumba za baba zao, 47 tangu waliopata umri wa miaka thelathini na zaidi, hata umri wa miaka hamsini, kila aliyeingia kufanya kazi ya utumishi, na kazi ya kuchukua mizigo katika hema ya kukutania, 48 hao waliohesabiwa kwao, walikuwa elfu nane na mia tano themanini. 49 Kwa amri ya Bwana, walihesabiwa kwa mkono wa Musa, kila mtu kwa utumishi wake, na kama mzigo wake ulivyokuwa; ndivyo walivyohesabiwa na yeye, kama Bwana alivyomwagiza Musa.

Hesabu 5

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Waamrishe wana wa Israeli kwamba wamtoe kila mwenye ukoma maragoni, na kila mtu aliye na kisonono, na kila aliye najisi kwa ajili ya wafu; 3 mtawatoa nje wote, waume kwa wake, mtawaweka nje ya marago; ili wasiyatie unajisi marago yao, ambayo mimi naketi katikati yake. 4 Wana wa Israeli wakafanya vivyo, wakawatoa na kuwaweka nje ya marago; kama Bwana alivyonena na Musa, ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. 5 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 6 Uwaambie wana wa Israeli, Mtu mume au mke atakapofanya dhambi yo yote, ifanywayo na binadamu, kumwasi Bwana, na mtu huyo akawa na hatia; 7 ndipo watakapoungama dhambi yao waliyoifanya; naye atarudisha kwa hatia yake, kwa utimilifu wake, tena ataongeza juu yake sehemu ya tano, na kumpa huyo aliyemkosa. 8 Lakini kwamba mtu huyo hana jamaa ya karibu ambaye inampasa kurudishiwa kwa ajili ya hiyo hatia, kile kitakachorudishwa kwa Bwana kwa hiyo hatia kitakuwa cha kuhani, pamoja na kondoo mume wa upatanisho, ambaye kwa huyo utafanywa upatanisho kwa ajili yake. 9 Tena kila sadaka ya kuinuliwa, ya vitu vitakatifu vya wana wa Israeli, watakavyosongeza kwa kuhani, itakuwa ni yake. 10 Tena vitu vilivyowekwa wakfu na mtu awaye yote, vitakuwa ni vya kuhani; kitu cho chote mtu atakachompa kuhani, kitakuwa chake. 11 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 12 Nena na wana wa israeli, uwaambie, kama mke wa mtu ye yote akikengeuka, na kumkosa mumewe, 13 na mtu mume akalala naye kwa uasherati, na jambo hilo likamfichamania mumewe, likawa jambo lisilojulikana, na huyo mwanamke akawa najisi, wala hapana shahidi aliyeshuhudia juu yake, wala hakufumaniwa; 14 kisha mumewe akashikwa na roho ya wivu, akamwonea wivu mkewe, naye akawa najisi huyo mwanamke; au kama akiingiwa na roho ya wivu, akamwonea wivu mkewe, naye hakuwa na unajisi huyo mke; 15 ndipo huyo mume atamchukua mkewe, aende naye kwa kuhani, naye ataleta sadaka yake kwa ajili yake, yaani, sehemu ya kumi ya efa ya unga wa shayiri; asitie mafuta juu yake, wala asitie ubani juu yake; maana, ni sadaka ya unga ya wivu, ni sadaka ya unga ya ukumbusho ya kukumbukia uovu. 16 Basi kuhani atamleta mwanamke akaribie, na kumweka mbele za Bwana; 17 kisha kuhani atatwaa maji matakatifu katika chombo cha udongo; kisha kuhani atatwaa katika vumbi lililo pale chini ya maskani, na kulitia katika hayo maji; 18 kisha kuhani atamweka mwanamke mbele za Bwana, naye atazifungua nywele za kichwani mwa huyo mwanamke, kisha atampa hiyo sadaka ya unga ya ukumbusho mikononi mwake, ambayo ni sadaka ya unga ya wivu, naye kuhani atakuwa na hayo maji ya uchungu yaletayo laana mkononi mwake; 19 tena kuhani atamwapisha huyo mwanamke, naye atamwambia mwanamke, Kwamba hakulala mtu mume pamoja nawe, tena kwamba hukukengeuka kuandama uchafu, uli chini ya mumeo, maji haya ya uchungu yaletayo laana yasikudhuru; 20 lakini kwamba umekengeuka uli chini ya mumeo, na kwamba u hali ya unajisi, na mtu mume amelala nawe, asiyekuwa mumeo; 21 hapo ndipo kuhani atamwapisha mwanamke kwa kiapo cha kuapiza, kisha kuhani atamwambia huyo mwanamke maneno haya, Bwana na akufanye wewe uwe laana na kiapo kati ya watu wako, hapo Bwana akufanyapo paja lako kupooza, na tumbo lako kuvimba; 22 na maji yaletayo laana yatakuingia matumboni mwako, na kukuvimbisha tumbo, na kukupoozesha paja lako; na mwanamke ataitika, Amina, Amina. 23 Kisha kuhani ataziandika laana hizo ndani ya kitabu, na kuzifuta katika maji ya uchungu; 24 kisha atamnywesha mwanamke hayo maji ya uchungu yaletayo laana; nayo maji yaletayo laana yataingia ndani yake, nayo yatageuka kuwa uchungu. 25 Kisha kuhani ataitwaa hiyo sadaka ya unga ya wivu, kwa kuiondoa mkononi mwa huyo mwanamke, naye ataitikisa sadaka ya unga mbele ya Bwana, na kuisongeza pale madhabahuni; 26 kisha kuhani atatwaa konzi moja ya sadaka ya unga, kuwa ni ukumbusho wake, na kuuteketeza madhabahuni, baadaye atamnywesha mwanamke hayo maji. 27 Kisha hapo atakapokwisha kumnywesha maji, ndipo itakapokuwa, kama amekuwa hali ya unajisi na kumkosa mumewe, hayo maji yaletayo laana yatamwingia ndani yake, nayo yatakuwa uchungu, na tumbo lake litavimba, na paja lake litapooza; na huyo mwanamke atakuwa laana kati ya watu wake. 28 Na kama mwanamke hakuwa na unajisi lakini yu safi; ndipo ataachiliwa, naye atazaa wana. 29 Hii ndiyo sheria ya wivu, mwanamke, ambaye yu chini ya mumewe, akikengeuka, na kupata unajisi; 30 au, roho ya wivu ikimwingia mtu mume, naye akamwonea wivu mkewe; ndipo atakapomweka huyo mwanamke mbele za Bwana, na kuhani atatenda juu yake sheria hii yote. 31 Na huyo mume atakuwa hana uovu, na mwanamke atauchukua uovu wake.

Hesabu 6

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na watu wa Israeli, uwaambie, Mtu mume au mtu mke atakapoweka nadhiri kubwa, nadhiri ya Mnadhiri, ili ajiweke wakfu kwa Bwana; 3 atajitenga na divai na vileo; hatakunywa siki ya divai, wala siki ya kileo, wala asinywe maji yo yote ya zabibu, wala asile zabibu, mbichi wala zilizokauka. 4 Siku zote za kujitenga kwake asile kitu cho chote kilichoandaliwa kwa mzabibu, tangu kokwa hata maganda. 5 Siku zote za nadhiri yake ya kujitenga, wembe usimfikilie kichwani mwake; hata hizo siku zitakapotimia, ambazo alijiweka wakfu kwa Bwana, atakuwa mtakatifu, ataziacha nywele za kichwani mwake zikue ziwe ndefu. 6 Siku hizo zote ambazo alijiweka awe wa Bwana asikaribie maiti. 7 Hatajitia unajisi kwa ajili ya baba yake, wala kwa ajili ya mamaye, wala kwa nduguye mume, wala kwa umbu lake, wakifa wao; kwa sababu ya huku kujiweka kwa Mungu ni juu ya kichwa chake. 8 Siku zote za kujitenga kwake, yeye ni mtakatifu kwa Bwana 9 Na kama mtu ye yote akifa ghafla karibu naye, akajitia unajisi kichwa cha kutengwa kwake, ndipo atakinyoa kichwa siku hiyo ya kutakaswa kwake, atakinyoa siku ya saba. 10 Tena siku ya nane ataleta hua wawili, au makinda mawili ya njiwa, aende nao kwa kuhani, hata mlangoni pa hema ya kukutania; 11 naye kuhani atasongeza mmoja kuwa sadaka ya dhambi, na wa pili kuwa sadaka ya kuteketezwa, naye atafanya upatanisho kwa ajili yake, kwa sababu aliingia kosani kwa ajili ya mfu, naye atatakasa kichwa chake siku iyo hiyo. 12 Kisha ataziweka kwa Bwana hizo siku za kujitenga kwake, naye ataleta mwana-kondoo mume wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya hatia; lakini hizo siku za kwanza hazitahesabiwa, kwa kuwa kule kujitenga kwake kulitiwa unajisi. 13 Na sheria ya Mnadhiri ni hii, zitakapotimia hizo siku za kujitenga kwake; ataletwa mlangoni pa hema ya kukutania; 14 naye atasongeza sadaka yake kwa Bwana, mwana-kondoo mmoja mume wa mwaka wa kwanza mkamilifu, kuwa sadaka ya kuteketezwa, na mwana-kondoo mmoja mke wa mwaka wa kwanza mkamilifu, kuwa sadaka ya dhambi, na kondoo mume mmoja mkamilifu kwa sadaka ya amani, 15 na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu, mikate ya unga mwembamba iliyokandwa kwa mafuta, na mikate ya kaki isiyochachwa, iliyotiwa mafuta, pamoja na sadaka zake za unga, na sadaka zake za kinywaji. 16 Na kuhani atavisongeza mbele za Bwana, naye atasongeza sadaka yake ya dhambi, na sadaka yake ya kuteketezwa; 17 naye atamsongeza huyo kondoo mume kuwa dhabihu ya sadaka za amani kwa Bwana, pamoja na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu; kisha kuhani atasongeza sadaka ya unga nayo, na sadaka yake ya kinywaji. 18 Naye Mnadhiri atakinyoa kichwa cha kujitenga kwake, mlangoni pa hema ya kukutania, kisha atatwaa hizo nywele za kichwa cha kujitenga kwake, na kuzitia katika moto ulio chini ya dhabihu ya sadaka za amani. 19 Kisha kuhani atautwaa mkono wa huyo kondoo mume uliotokoswa, na mkate mmoja usio chachu atautwaa kikapuni, na mkate mmoja wa kaki, naye ataitia mikononi mwa yule Mnadhiri, baada ya kunyoa kichwa cha kujitenga kwake; 20 naye kuhani atavitikisa viwe sadaka ya kutikiswa mbele za Bwana; kitu hicho ni kitakatifu kwa kuhani, pamoja na kidari cha kutikiswa, na paja la kuinuliwa; kisha baadaye Mnadhiri ana ruhusa kunywa divai. 21 Sheria ya Mnadhiri awekaye nadhiri ni hiyo, tena ni sheria ya sadaka yake atakayomtolea Bwana kwa ajili ya kujitenga kwake, pamoja na vitu vile ambavyo aweza kuvipata zaidi; kama nadhiri yake awekayo ilivyo, ndivyo impasavyo kufanya kwa kuiandama sheria ya kujitenga kwake. 22 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 23 Nena na Haruni na wanawe, uwaambie, Hivi ndivyo mtakavyowabarikia wana wa Israeli; mtawaambia; 24 Bwana akubarikie, na kukulinda; 25 Bwana akuangazie nuru za uso wake, na kukufadhili; 26 Bwana akuinulie uso wake, na kukupa amani. 27 Ndivyo watakavyoweka jina langu juu ya wana wa Israeli; nami nitawabarikia.

Hesabu 7

1 Ilikuwa siku hiyo Musa alipokwisha kuisimamisha maskani, na kuitia mafuta, na kuitakasa, na vyombo vyake vyote, na hiyo madhabahu na vyombo vyake vyote, na kuvitia mafuta, na kuvitakasa; 2 ndipo wakuu wa Israeli, vichwa vya nyumba za baba zao, wakatoa matoleo; hao ndio wakuu wa kabila, hao ndio waliokuwa juu yao waliohesabiwa; 3 nao wakamletea Bwana matoleo yao, magari sita yenye mafuniko juu, na ng'ombe kumi na wawili; gari moja kwa wakuu wawili wawili, na ng'ombe mmoja kwa kila mkuu; nao wakayasongeza hapo mbele ya maskani. 4 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 5 Pokea mikononi mwao, ili kwamba viwe vya kutumiwa katika utumishi wa hema ya kukutania; nawe utawapa Walawi vitu hivyo, kila mtu utampa kama utumishi wake ulivyo. 6 Basi Musa akapokea hayo magari, na ng'ombe, akawapa Walawi. 7 Wana wa Gershoni akawapa magari mawili na ng'ombe wanne, kama utumishi wao ulivyokuwa; 8 na wana wa Merari akawapa magari manne na ng'ombe wanane kama utumishi wao ulivyokuwa, chini ya mkono wa Ithamari, mwana wa Haruni kuhani. 9 Lakini hakuwapa wana wa Kohathi; maana, utumishi wa vile vitu vitakatifu ulikuwa ni wao; nao wakavichukua mabegani mwao. 10 Kisha wale wakuu wakatoa matoleo kwa ajili ya kuiweka wakfu madhabahu, katika siku hiyo iliyotiwa mafuta, wakuu wakayatoa matoleo yao mbele ya madhabahu. 11 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, Watasongeza matoleo yao, kila mkuu kwa siku yake, kwa ajili ya kuiweka wakfu madhabahu. 12 Basi aliyetoa matoleo yake siku ya kwanza ni Nashoni mwana wa Aminadabu, wa kabila ya Yuda; 13 na matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha uzani wake ni shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta kuwa sadaka ya unga; 14 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kimejaa uvumba; 15 ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mmoja mume, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 16 mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 17 na kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe waume wawili, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Nashoni mwana wa Aminadabu. 18 Siku ya pili Nethaneli mwana wa Suari, mkuu wa Isakari, alitoa; 19 yeye akasongeza matoleo yake, sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa ni sadaka ya unga; 20 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilikuwa kimejaa uvumba; 21 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 22 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 23 na kwa dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Nethaneli mwana wa Suari. 24 Siku ya tatu Eliabu mwana wa Heloni, mkuu wa wana wa Zabuloni; 25 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 26 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 27 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 28 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 29 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Eliabu mwana wa Heloni. 30 Siku ya nne Elisuri mwana wa Shedeuri, mkuu wa wana wa Reubeni; 31 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 32 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 33 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 34 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 35 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Elisuri mwana wa Shedeuri. 36 Siku ya tano Shelumieli mwana wa Suri-shadai, mkuu wa wana Simeoni; 37 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 38 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 39 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 40 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 41 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Shelumieli mwana wa Suri-shadai 42 Siku ya sita Eliasafu mwana wa Deueli, mkuu wa wana wa Gadi 43 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 44 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 45 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 46 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 47 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Eliasafu mwana wa Deueli. 48 Siku ya saba Elishama mwana wa Amihudi, mkuu wa wana wa Efraimu; 49 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 50 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 51 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 52 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 53 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Elishama mwana wa Amihudi. 54 Siku ya nane Gamalieli mwana wa Pedasuri, mkuu wa wana wa Manase; 55 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 56 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 57 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 58 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 59 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Gamalieli mwana wa Pedasuri. 60 Siku ya kenda Abidani mwana wa Gideoni, mkuu wa wana wa Benyamini; 61 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 62 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 63 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 64 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 65 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Abidani mwana wa Gideoni. 66 Siku ya kumi Ahiezeri mwana wa Amishadai, mkuu wa wana wa Dani; 67 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 68 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 69 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 70 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 71 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Ahiezeri mwana wa Amishadai. 72 Na siku ya kumi na moja Pagieli mwana wa Okrani, mkuu wa wana wa Asheri; 73 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 74 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 75 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 76 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 77 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Pagieli mwana wa Okrani. 78 Na siku ya kumi na mbili Ahira mwana wa Enani, mkuu wa wana wa Naftali; 79 matoleo yake yalikuwa sahani moja ya fedha, uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na bakuli moja ya fedha, uzani wake shekeli sabini, kwa shekeli ya mahali patakatifu; vyombo hivyo vyote viwili vilikuwa vimejaa unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, kuwa sadaka ya unga; 80 na kijiko kimoja cha dhahabu, uzani wake shekeli kumi, kilichojaa uvumba; 81 na ng'ombe mmoja mume mchanga, na kondoo mume mmoja, na mwana-kondoo mume mmoja wa mwaka wa kwanza, kuwa sadaka ya kuteketezwa; 82 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; 83 tena kwa ajili ya dhabihu ya sadaka za amani, ng'ombe wawili waume, na kondoo waume watano, na mbuzi waume watano, na wana-kondoo watano waume wa mwaka wa kwanza; hayo ndiyo matoleo ya Ahira mwana wa Enani. 84 Hayo ndiyo matoleo yaliyotolewa na wakuu wa Israeli kwa ajili ya kuiweka wakfu madhabahu, siku hiyo ilipotiwa mafuta; sahani za fedha kumi na mbili, na bakuli za fedha kumi na mbili, na vijiko vya dhahabu kumi na viwili; 85 kila sahani ya fedha uzani wake ni shekeli mia na thelathini, na kila bakuli uzani wake ni shekeli sabini; fedha yote ya vile vyombo ilikuwa shekeli elfu mbili na mia nne, kwa shekeli ya mahali patakatifu; 86 na vijiko vya dhahabu vilivyojaa uvumba kumi na viwili, uzani wake kila kijiko shekeli kumi, kwa shekeli ya mahali patakatifu; dhahabu yote ya vile vijiko ilikuwa shekeli mia na ishirini; 87 ng'ombe wote waliokuwa wa sadaka ya kuteketezwa walikuwa ng'ombe waume kumi na wawili, na hao kondoo waume walikuwa kumi na wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza walikuwa kumi na wawili, pamoja na sadaka yao ya unga; na mbuzi waume wa sadaka ya dhambi ni kumi na wawili; 88 na ng'ombe wote waliokuwa wa dhabihu ya sadaka za amani ni ng'ombe waume ishirini na wanne, na hao kondoo waume walikuwa ni sitini, na hao mbuzi waume walikuwa ni sitini, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza walikuwa sitini. Hayo ndiyo matoleo yaliyotolewa kwa ajili ya kuiweka wakfu madhabahu, baada ya hiyo madhabahu kutiwa mafuta. 89 Kisha, Musa alipoingia ndani ya hema ya kukutania ili kunena na Mungu ndipo alipoisikia Sauti ikinena naye kutoka hapo juu ya kiti cha rehema, kilichokuwa juu ya sanduku la ushahidi, ikitoka kati ya yale makerubi mawili; naye akanena naye.

Hesabu 8

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na Haruni, ukamwambie, Utakapoziweka taa, hizo taa saba zitatoa nuru hapo mbele ya kinara cha taa. 3 Basi Haruni akafanya; akaziweka taa zake ili zitoe nuru hapo mbele ya kinara, kama Bwana alivyomwagiza Musa. 4 Na hii ndiyo kazi ya hicho kinara cha taa, ilikuwa ni kazi ya ufuzi wa dhahabu; tangu tako lake hata maua yake kilikuwa ni kazi ya ufuzi; vile vile kama ule mfano Bwana aliokuwa amemwonyesha Musa, ndivyo alivyokifanya kinara. 5 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 6 Watwae Walawi na kuwaondoa kati ya wana wa Israeli, kisha uwatakase. 7 Nawe utawafanyia mambo haya ili kuwatakasa; nyunyiza juu yao maji yatakasayo dhambi, nao wajinyoe kwa wembe mwili wote, kisha wazifue nguo zao, na kujitakasa. 8 Kisha na watwae ng'ombe mume mmoja mchanga, na sadaka yake ya unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, nawe utatwaa ng'ombe mume mchanga mwingine kuwa sadaka ya dhambi. 9 Nawe utawahudhurisha Walawi mbele ya hema ya kukutania; nawe utaukutanisha mkutano wote wa wana wa Israeli; 10 nawe utawahudhurisha Walawi mbele za Bwana; kisha wana wa Israeli wataweka mikono yao juu ya Walawi; 11 naye Haruni atawasongeza Walawi mbele za Bwana wawe sadaka ya kutikiswa, kwa ajili ya wana wa Israeli, ili wawe wenye kufanya utumishi wa Bwana. 12 Kisha Walawi wataweka mikono yao juu ya vichwa vya hao ng'ombe; nawe umtoe mmoja kuwa sadaka ya dhambi kwa Bwana, na huyo wa pili awe sadaka ya kuteketezwa, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya Walawi. 13 Kisha utawaweka Walawi mbele ya Haruni, na mbele ya wanawe na kuwasongeza kwa Bwana wawe sadaka ya kutikiswa. 14 Ndivyo utakavyowatenga Walawi na kuwatoa katika wana wa Israeli; na Walawi watakuwa wangu. 15 Kisha baadaye Walawi wataingia ndani, ili wafanye utumishi wa hema ya kukutania; nawe utawatakasa, na kuwasongeza wawe sadaka ya kutikiswa. 16 Kwa kuwa nimepewa kabisa mimi watu hawa kutoka katika wana wa Israeli; badala ya wote wafunguao mimba, maana, wazaliwa wa kwanza wa wana wa Israeli wote, nimewatwaa wawe wangu. 17 Kwa kuwa wazaliwa wa kwanza wote katika wana wa Israeli ni wangu, wa wanadamu na wa wanyama; siku hiyo niliyowapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri niliwatakasa kwa ajili yangu mwenyewe. 18 Nami nimewatwaa Walawi badala ya wazaliwa wa kwanza wote walio katika wana wa Israeli. 19 Nami nimempa Haruni hao Walawi wawe kipawa chake yeye na wanawe, kutoka kwa wana wa Israeli, ili watumike utumishi wa wana wa Israeli katika hema ya kukutania, kisha wafanye upatanisho kwa ajili ya wana wa Israeli; ili kusiwe na maradhi kati ya wana wa Israeli, hapo wana wa Israeli watakapopakaribia mahali patakatifu. 20 Basi Musa na Haruni, na mkutano wote wa wana wa Israeli, wakawafanyia Walawi mambo hayo; kama hayo yote Bwana aliyomwagiza Musa kwa habari za hao Walawi, ndivyo wana wa Israeli walivyowafanyia. 21 Walawi wakajitakasa na dhambi, nao wakafua nguo zao; kisha Haruni akawasongeza mbele za Bwana wawe sadaka ya kutikiswa; Haruni akafanya kwa ajili yao ili kuwatakasa. 22 Kisha baada ya hayo Walawi wakaingia ili wafanye utumishi wao ndani ya hema ya kukutania mbele ya Haruni na mbele ya wanawe; kama Bwana alivyomwagiza Musa kwa habari za hao Walawi, ndivyo walivyowafanyia. 23 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 24 Mambo yawapasayo hao Walawi ni haya; tangu waliopata umri wa miaka ishirini na mitano na zaidi wataingia ndani ili watumike utumishi katika kazi ya hema ya kukutania; 25 tena tangu waliopata umri wa miaka hamsini wataacha kutumika huo utumishi, wasitumike tena; 26 lakini watatumika pamoja na ndugu zao katika hema ya kukutania, kushika ulinzi, lakini wasitumike katika huo utumishi tena. Ndivyo utakavyowafanyia Walawi katika mambo ya ulinzi wao.

Hesabu 9

1 Kisha Bwana akanena na Musa katika bara ya Sinai, mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili baada ya kutoka kwao katika nchi ya Misri, akamwambia, 2 Tena, wana wa Israeli na washike sikukuu ya Pasaka kwa wakati wake ulioagizwa. 3 Siku ya kumi na nne ya mwezi huu, wakati wa jioni, mtaishika kwa wakati wake ulioagizwa; kwa amri zake zote, na kama hukumu zake zote zilivyo, ndivyo mtakavyoishika. 4 Kisha Musa akawaambia wana wa Israeli kwamba waishike sikukuu hiyo ya Pasaka; 5 Nao wakaishika Pasaka katika mwezi wa kwanza, siku ya kumi na nne ya mwezi, wakati wa jioni, katika bara ya Sinai vile vile kama hayo yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. 6 Basi walikuwako watu waume kadha wa kadha waliokuwa na unajisi kwa ajili ya maiti wa mtu, hata wasiweze kuishika Pasaka siku hiyo; nao wakaenda mbele ya Musa na Haruni, siku hiyo hao watu wakamwambia, 7 Sisi tu hali ya unajisi kwa ajili ya maiti wa mtu; nasi tumezuiwa kwa nini hata tusipate kumtolea Bwana matoleo kwa wakati wake ulioagizwa, kati ya wana wa Israeli? 8 Musa akawaambia, Ngojeni hapo; hata nipate sikiza Bwana atakaloagiza juu yenu. 9 Bwana akanena na Musa, akamwambia, 10 Nena na wana wa Israeli, kuwaambia, Mtu wa kwenu, au wa vizazi vyenu, ye yote atakayekuwa na unajisi kwa ajili ya maiti, au akiwako mbali katika safari, na haya yote, ataishika Pasaka kwa Bwana; 11 mwezi wa pili, siku ya kumi na nne ya mwezi, wakati wa jioni, wataishika; watamla pamoja na mikate isiyotiwa chachu na mboga za uchungu; 12 wasisaze kitu chake cho chote hata asubuhi, wala wasimvunje mfupa wake; kama hiyo sheria yote ya Pasaka ilivyo ndivyo watakavyoishika. 13 Lakini mtu aliye safi, wala hakuwa katika safari, naye amekosa kuishika Pasaka, mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake; kwa sababu hakumtolea Bwana matoleo kwa wakati wake ulioamriwa, mtu huyo atachukua dhambi yake. 14 Na kama mgeni akiketi kati yenu ugenini, naye ataka kuishika Pasaka kwa Bwana; kama hiyo sheria ya Pasaka ilivyo, na kama amri yake ilivyo, ndivyo atakavyofanya; mtakuwa na sheria moja, kwa huyo aliye mgeni, na kwa huyo aliyezaliwa katika nchi. 15 Na siku hiyo maskani iliposimamishwa, lile wingu likaifunika maskani, yaani, hema ya kukutania; wakati wa jioni likawa juu ya maskani, mfano wa moto, hata asubuhi. 16 Ndivyo ilivyokuwa sikuzote; lile wingu liliifunika kwa mfano wa moto usiku. 17 Na kila lilipoinuliwa lile wingu juu ya ile Hema ndipo wana wa Israeli waliposafiri; na mahali lilipokaa lile wingu, ndipo wana wa Israeli walipopiga kambi yao. 18 Kwa amri ya Bwana Wana wa Israeli walisafiri, na kwa amri ya Bwana walipiga kambi; wakati lile wingu ilipokaa juu ya maskani walikaa katika kambi yao. 19 Na lile wingu lilipokawia juu ya maskani siku nyingi, ndipo wana wa Israeli walipolinda malinzi ya Bwana, wala hawakusafiri. 20 Na pengine lile wingu lilikaa juu ya maskani siku chache; ndipo kwa amri ya Bwana walikaa katika kambi yao, tena kwa amri ya Bwana walisafiri. 21 Na pengine lile wingu lilikaa tangu jioni hata asubuhi; na lile wingu lilipoinuliwa asubuhi walisafiri, au kama likikaa usiku na mchana pia, lilipoinuliwa lile wingu, ndipo waliposafiri. 22 Ikiwa lile wingu lilikawia, likikaa juu ya maskani siku mbili, au mwezi, au mwaka, wana wa Israeli walikaa katika kambi yao, wasisafiri; 23 bali lilipoinuliwa walisafiri. Kwa amri ya Bwana walipiga kambi yao, na kwa amri ya Bwana walisafiri; wakayalinda malinzi ya Bwana, kwa mkono wa Musa.

Hesabu 10

1 Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia, 2 Jifanyie tarumbeta mbili za fedha; utazifanya za kazi ya ufuzi; nawe utazitumia kwa kuwaita mkutano wakutane, na kwa kusafiri kwao yale makambi. 3 Na hapo watakapozipiga hizo tarumbeta, mkutano wote utakukutanikia wewe, hapo mlangoni pa hema ya kukutania. 4 Nao wakipiga tarumbeta moja tu ndipo wakuu, walio vichwa vya maelfu ya Israeli, watakukutanikia wewe 5 Tena hapo mtakapopiga sauti ya kugutusha sana, marago yaliyoko upande wa mashariki yatasafiri. Tena hapo mtakapopiga sauti ya kugutusha ya pili, marago yaliyoko upande wa kusini watasafiri; 6 watapiga sauti ya kugutusha kwa ajili ya safari zao. 7 Lakini mkutano utakapokutanishwa pamoja mtapiga, lakini hamtapiga sauti ya kugutusha. 8 Wana wa Haruni, makuhani, ndio watakaopiga hizo tarumbeta; nazo zitakuwa kwenu ni amri ya milele katika vizazi vyenu vyote. 9 Tena hapo mtakapokwenda kupiga vita katika nchi yenu, kupigana na adui awaoneaye ninyi, ndipo mtakapopiga sauti ya kugutusha kwa tarumbeta; nanyi mtakumbukwa mbele za Bwana, Mungu wenu, nanyi mtaokolewa na adui zenu. 10 Tena katika siku ya furaha yenu, na katika sikukuu zenu zilizoamriwa, na katika kuandama miezi kwenu, mtapiga hizo tarumbeta juu ya sadaka zenu za kuteketezwa, na juu ya dhabihu za sadaka zenu za amani; nazo zitakuwa kwenu ni ukumbusho mbele za Mungu wenu; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 11 Ikawa mwaka wa pili, mwezi wa pili, siku ya ishirini ya mwezi, hilo wingu liliinuka kutoka pale juu ya maskani ya ushahidi. 12 Wana wa Israeli wakasafiri kwenda mbele, kwa safari zao kutoka jangwa la Sinai; na hilo wingu likakaa katika jangwa la Parani. 13 Nao wakasafiri kwanza kwa amri ya Bwana kwa mkono wa Musa. 14 Mahali pa mbele ilisafiri beramu ya marago ya wana wa Yuda, kwa majeshi yao; na Nashoni mwana wa Aminadabu ndiye aliyekuwa juu ya jeshi lake. 15 Na juu ya jeshi la kabila ya wana wa Isakari alikuwa Nethaneli mwana wa Suari. 16 Na juu ya jeshi la kabila ya wana wa Zabuloni ni Eliabu mwana wa Heloni. 17 Na maskani ilishushwa; na wana wa Gershoni, na wana wa Merari, walioichukua maskani, wakasafiri kwenda mbele. 18 Kisha beramu ya marago ya Reubeni ikasafiri kwenda mbele kwa majeshi yao; na juu ya jeshi lake alikuwa Elisuri mwana wa Shedeuri. 19 Tena juu ya jeshi la kabila ya wana wa Simeoni ni Shelumieli mwana wa Suri-shadai. 20 Tena juu ya jeshi la kabila ya wana wa Gadi ni Eliasafu mwana wa Deueli. 21 Ndipo wakasafiri Wakohathi wenye kuvichukua vile vitu vitakatifu; na hao wengine wakaisimamisha maskani kabla hawajaja wao. 22 Kisha beramu ya marago ya wana wa Efraimu ikasafiri kwenda mbele kwa majeshi yao; na juu ya jeshi lake ni Elishama mwana wa Amihudi. 23 Tena juu ya jeshi la kabila ya wana wa Manase ni Gamalieli mwana wa Pedasuri. 24 Tena juu ya jeshi la kabila ya wana wa Benyamini ni Abidani mwana wa Gideoni. 25 Kisha beramu ya marago ya wana wa Dani, ambayo yalikuwa ni nyuma ya marago yote, ikasafiri, kwa majeshi yao; na juu ya jeshi lake ni Ahiezeri mwana wa Amishadai. 26 Tena juu ya jeshi la kabila ya wana wa Asheri ni Pagieli mwana wa Okrani; 27 Tena juu ya jeshi la kabila ya wana wa Naftali ni Ahira mwana wa Enani. 28 Ndivyo zilivyokuwa safari zao wana wa Israeli kwa majeshi: yao; nao wakasafiri kwenda mbele. 29 Kisha Musa akamwambia Hobabu, mwana wa Reueli Mmidiani, mkwewe Musa, Sisi twasafiri kwenenda mahali ambapo Bwana amenena habari zake hivi, Nitawapa ninyi mahali hapo; uje pamoja nasi, nasi tutakufanyia mema; kwa kuwa Bwana ametamka mema juu ya Israeli. 30 Naye akamwambia, Siendi mimi; ila nitairudia nchi yangu mwenyewe, na kwa jamaa zangu mwenyewe. 31 Naye akamwambia, Usituache, tafadhali; kwa kuwa wewe wajua jinsi tutakavyopanga nyikani, nawe utakuwa kwetu badala ya macho. 32 Itakuwa, ukienda pamoja nasi, naam, itakuwa mema yo yote Bwana atakayotutendea sisi, tutakutendea wewe vivyo. 33 Basi wakasafiri kutoka penye mlima wa Bwana safari ya siku tatu; na sanduku la agano la Bwana likatangulia mbele yao mwendo wa siku tatu, ili kuwatafutia mahali pa kupumzika. 34 Na wingu la Bwana lilikuwa juu yao mchana hapo waliposafiri kwenda mbele kutoka kambini. 35 Ilikuwa, hapo sanduku liliposafiri kwenda mbele, ndipo Musa akasema, Inuka, Ee Bwana, adui zako na watawanyike; na wakimbie mbele zako hao wakuchukiao. 36 Tena hapo liliposimama, akasema, Ee Bwana, uwarudie maelfu kumi ya maelfu ya Israeli.

Hesabu 11

1 Kisha hao watu walikuwa kama wanung'unikao, wakinena maovu masikioni mwa Bwana; Bwana aliposikia hayo, hasira zake zikawaka; na moto wa Bwana ukawaka kati yao, ukateketeza katika mipaka ya mwisho wa marago. 2 Ndipo watu wakamlilia Musa; naye Musa akamwomba Bwana, na ule moto ukakoma. 3 Jina la mahali hapo likaitwa Tabera; kwa sababu huo moto wa Bwana ukawaka kati yao. 4 Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N'nani atakayetupa nyama tule? 5 Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; 6 lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu. 7 Na hiyo mana ilikuwa mfano wa chembe za mtama na kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwake bedola. 8 Watu wakazunguka-zunguka na kuikusanya, kisha wakaisaga kwa mawe ya kusagia, au kuitwanga katika vinu, kisha wakaitokosa nyunguni, na kuandaa mikate; na tamu yake ilikuwa kama tamu ya mafuta mapya. 9 Umande ulipoyaangukia marago wakati wa usiku, hiyo mana ilianguka pamoja nao. 10 Basi Musa akawasikia watu wakilia katika jamaa zao zote, kila mtu mlangoni pa hema yake; na hasira za Bwana zikawaka sana; Musa naye akakasirika. 11 Musa akamwambia Bwana, Mbona umenitenda uovu mimi mtumishi wako? Kwa nini sikupata neema machoni pako, hata ukanitwika mzigo wa watu hawa wote juu yangu? 12 Je! Ni mimi niliyewatungisha mimba watu hawa wote je! Ni mimi niliyewazaa, hata ikawa wewe kuniambia, Haya, wachukue kifuani mwako, mfano wa baba mwenye kulea achukuavyo mtoto anyonyaye, uende nao mpaka nchi uliyowaapia baba zao? 13 Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula. 14 Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda. 15 Na kama ukinitenda hivi, nakuomba uniulie mbali, kwamba nimepata fadhili mbele ya macho yako; nami nisiyaone haya mashaka yangu. 16 Kisha Bwana akamwambia Musa, Nikusanyie watu sabini, miongoni mwa wazee wa israeli, ambao wewe wawajua kuwa ndio wazee wa watu hawa, na maakida juu yao; ukawalete hata hema ya kukutania, wasimame huko pamoja nawe. 17 Nami nitashuka niseme nawe huko, nami nitatwaa sehemu ya roho iliyo juu yako na kuiweka juu yao; nao watachukua mzigo wa watu hawa pamoja nawe, ili usiuchukue wewe peke yako. 18 Kisha uwaambie watu hawa, Jitakaseni nafsi zenu kabla ya kesho, nanyi mtakula nyama; kwa maana mmelia masikioni mwa Bwana, mkisema, Ni nani atakayetupa nyama, tule? Maana huko Misri tulikuwa na uheri. Basi kwa sababu hiyo Bwana atawapa nyama, nanyi mtakula. 19 Hamtakula siku moja, wala siku mbili, wala siku tano, wala siku kumi, wala siku ishirini; 20 lakini mtakula muda wa mwezi mzima, hata hapo nyama hiyo itakapotoka katika mianzi ya pua zenu, nanyi mtaikinai, kwa sababu mmemkataa Bwana aliye kati yenu, na kulia mbele zake, mkisema, Tulitoka Misri kwa maana gani? 21 Musa akasema, Watu hawa ambao mimi ni kati yao, ni watu sita mia elfu waendao kwa miguu; nawe umesema, Nitawapa nyama, ili wale muda wa mwezi mzima. 22 Je! Makundi ya kondoo na ng'ombe yatachinjwa kwa ajili yao, ili kuwatosha? Au samaki wote wa baharini watakusanywa pamoja kwa ajili yao, ili kuwatosha? 23 Bwana akamwambia Musa, Je! Mkono wa Bwana umepungua urefu wake? Sasa utaona kwamba neno langu litatimizwa kwako, au sivyo. 24 Musa akatoka, akawaambia watu maneno ya Bwana; akawakutanisha watu sabini miongoni mwa wazee wa watu, akawaweka kuizunguka Hema. 25 Ndipo Bwana akashuka ndani ya wingu, akanena naye, akatwaa sehemu ya roho iliyokuwa juu ya Musa, akaitia juu ya wale wazee sabini; ikawa, roho hiyo ilipowashukia, wakatabiri, lakini hawakufanya hivyo tena. 26 Lakini watu wawili walisalia kambini, jina la mmoja aliitwa Eldadi, na jina la wa pili aliitwa Medadi; na roho ile ikawashukia; nao walikuwa miongoni mwao walioandikwa, lakini walikuwa hawakutoka kwenda hemani; nao wakatabiri kambini. 27 Mtu mmoja kijana akapiga mbio, akaenda akamwambia Musa, akasema, Eldadi na Medadi wanatoa unabii kambini. 28 Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa tangu ujana wake, akajibu akasema, Ee bwana wangu Musa, uwakataze. 29 Musa akamwambia, Je! Umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa Bwana wangekuwa manabii na kama Bwana angewatia roho yake. 30 Kisha Musa akaenda akaingia kambini, yeye na wale wazee wa Israeli. 31 Kisha upepo ukavuma kutoka kwa Bwana, nao ukaleta kware kutoka pande za baharini, nao ukawaacha wakaanguka karibu na kambi, kama kiasi cha mwendo wa siku moja upande huu, na kama kiasi cha mwendo wa siku moja upande huu, kuizunguka, nao wakafikilia kiasi cha dhiraa mbili juu ya uso wa nchi. 32 Watu wakaondoka mchana huo wote, na usiku huo wote, na siku ya pili yote, kuwakusanya hao kware; yeye aliyepata ya upungufu kuliko wenziwe alipata kiasi cha homeri kumi; nao wakawaanika wote kando-kando ya kambi kuizunguka pande zote. 33 Kisha hapo hiyo nyama ilipokuwa ikali kati ya meno yao, hawajaitafuna bado, hasira za Bwana ziliwaka juu ya watu, Bwana akawapiga watu kwa pigo kuu mno. 34 Jina la mahali pale likaitwa Kibroth-hataava; maana, ni hapo walipowazika hao watu waliotamani. 35 Kutoka hapo Kibroth-hataava watu wakasafiri kwenda Haserothi; wakakaa huko Haserothi.

Hesabu 12

1 Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi. 2 Wakasema, Je! Ni kweli Bwana amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao. 3 Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi. 4 Bwana akanena ghafula na Musa, na Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje. 5 Bwana akashuka katika nguzo ya wingu akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili. 6 Kisha akawaambia,Sikizeni basi maneno yangu;Akiwapo nabii kati yenu,Mimi,Bwana,nitajifunua kwake katika maono,Nitasema naye katika ndoto. 7 Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; 8 Kwake nitanena mdomo kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? 9 Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake. 10 Kisha hilo wingu likaondoka kutoka pale juu ya hema; na tazama, Miriamu akawa mwenye ukoma, mweupe kama theluji; Haruni akamwangalia Miriamu, na tazama, yu mwenye ukoma. 11 Kisha Haruni akamwambia Musa, Ee bwana wangu nakusihi sana usituwekee dhambi juu yetu, kwa kuwa tumefanya ya upumbavu, na kufanya dhambi. 12 Nakusihi, asiwe kama mmoja aliyekufa, ambaye nyama ya mwili wake nusu imelika hapo atokapo tumbo la mama yake. 13 Musa akamlilia Bwana, akasema, Mpoze, Ee Mungu, nakusihi sana. 14 Bwana akamwambia Musa, Je! Kama baba yake angalimtemea mate usoni tu, hangaliona aibu muda wa siku saba? Na afungwe nje ya kambi muda wa siku saba, kisha baada ya hayo ataletwa ndani tena. 15 Basi Miriamu alifungwa nje ya kambi muda wa siku saba; wala watu hawakusafiri hata Miriamu alipoletwa ndani tena. 16 Baada ya hayo watu wakasafiri kutoka Haserothi, wakapanga kambi katika nyika ya Parani.

Hesabu 13

1 Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia, 2 Tuma watu, ili waende wakaipeleleze nchi ya Kanaani, niwapayo wana wa Israeli; katika kabila ya baba zao mtamtuma mtu mmoja, kila mtu na awe mkuu kati yao. 3 Basi Musa akawatuma kutoka nyika ya Parani kama alivyoagizwa na Bwana; wote walikuwa ni watu walio vichwa vya wana wa Israeli. 4 Na majina yao ni haya; katika kabila ya Reubeni, Shamua mwana Zakuri. 5 Katika kabila ya Simeoni, Shafati mwana wa Hori. 6 Katika kabila ya Yuda, Kalebu mwana wa Yefune. 7 Katika kabila ya Isakari, Igali mwana wa Yusufu. 8 Katika kabila ya Efraimu, Hoshea mwana wa Nuni 9 Katika kabila ya Benyamini, Palti mwana wa Rafu. 10 Katika kabila ya Zabuloni, Gadieli mwana wa Sodi. 11 Katika kabila ya Yusufu, yaani, katika kabila ya Manase, Gadi mwana wa Susi. 12 Katika kabila ya Dani, Amieli mwana wa Gemali. 13 Katika kabila ya Asheri, Sethuri mwana wa Mikaeli. 14 Katika kabila ya Naftali, Nabi mwana wa Wofsi. 15 Katika kabila ya Gadi, Geueli mwana wa Maki. 16 Hayo ndiyo majina ya hao watu waliotumwa na Musa waende kuipeleleza nchi. Na huyo Hoshea mwana wa Nuni, Musa akamwita jina lake Yoshua. 17 Musa akawapeleka ili waipeleleze nchi ya Kanaani, akawaambia, Pandeni sasa katika Negebu mkapande milimani, 18 mkaitazame nchi ni ya namna gani; na watu wanaokaa ndani yake, kwamba ni hodari au dhaifu, kwamba ni wachache au wengi; 19 na nchi wanayoikaa kwamba ni njema au mbaya; kwamba wanakaa katika matuo au katika ngome; 20 nayo nchi ni ya namna gani, kwamba ni nchi ya unono au ya njaa, kwamba ina msitu au sivyo. Iweni na moyo mkuu, mkayalete matunda ya nchi. Basi wakati ule ulikuwa wakati wa kuiva zabibu za kwanza. 21 Basi wakapanda wakaipeleleza nchi toka jangwa la Sini hata Rehobu, mpaka kuingia Hamathi. 22 Wakapanda katika Negebu, wakafika Hebroni; na Ahimani, na Sheshai, na Talmai, wana wa Anaki, walikuwako huko. Nao Hebroni ulijengwa miaka saba kabla ya Soani wa Misri. 23 Wakafika bonde la Eshkoli, na huko wakakata tawi lenye kishada kimoja cha zabibu, wakalichukua kwa mti kati ya watu wawili; wakaleta makomamanga pia, na tini. 24 Bonde lile liliitwa bonde la Eshkoli kwa sababu ya hicho kishada walichokata huko wana wa Israeli. 25 Wakarejea baada ya kuipeleleza nchi, mwisho wa siku arobaini. 26 Wakaenda wakafika kwa Musa, na kwa Haruni, na kwa mkutano wote wa wana wa Israeli, katika jangwa la Parani, huko Kadeshi; wakawaletea habari, wao na mkutano wote, wakawaonyesha matunda ya nchi. 27 Wakamwambia wakasema, Tulifika nchi ile uliyotutuma, na hakika yake, ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali, na haya ndiyo matunda yake. 28 Lakini watu wanaokaa katika nchi ile ni hodari, na miji yao ina maboma, nayo ni makubwa sana; na pamoja na hayo tuliwaona wana wa Anaki huko. 29 Amaleki anakaa katika nchi ya Negebu; na Mhiti, na Myebusi, na Mwamori wanakaa katika milima, na Mkanaani anakaa karibu na bahari; na kando ya ukingo wa Yordani. 30 Kalebu akawatuliza watu mbele ya Musa, akasema, Na tupande mara, tukaitamalaki; maana twaweza kushinda bila shaka. 31 Bali wale watu waliopanda pamoja naye wakasema, Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi. 32 Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza, wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno. 33 Kisha, huko tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi.

Hesabu 14

1 Mkutano wote wakapaza sauti zao wakalia; watu wakatoka machozi usiku ule. 2 Kisha wana wa Israeli wote wakamnung'unikia Musa na Haruni; mkutano wote wakawaambia, Ingekuwa heri kama tungalikufa katika nchi ya Misri, au, ingekuwa heri kama tungalikufa katika jangwa hili. 3 Mbona Bwana anatuleta mpaka nchi hii ili tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu watakuwa mateka; je! Si afadhali turudi Misri? 4 Wakaambiana, Na tumweke mtu mmoja awe akida, tukarudi Misri. 5 Ndipo Musa na Haruni wakaanguka kifudifudi mbele ya mkutano wa kusanyiko la wana wa Israeli. 6 Na Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwao walioipeleleza nchi, wakararua nguo zao; 7 wakanena na mkutano wote wa wana wa Israeli wakasema, Nchi ile tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi njema mno ya ajabu. 8 Ikiwa Bwana anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. 9 Lakini msimwasi Bwana, wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi, maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye Bwana yu pamoja nasi; msiwaogope. 10 Lakini mkutano wote wakaamuru wapigwe kwa mawe. Ndipo utukufu wa Bwana ukaonekana katika hema ya kukutania, mbele ya wana wa Israeli wote. 11 Bwana akamwuliza Musa, Je! Watu hawa watanidharau hata lini? Wasiniamini hata lini? Nijapokuwa nimefanya ishara hizo zote kati yao. 12 Nitawapiga kwa tauni, na kuwaondolea urithi wao, nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, kisha yenye nguvu kuliko wao. 13 Basi Musa akamwambia Bwana, Ndipo Wamisri watasikia habari hiyo; kwa kuwa wewe uliwaleta watu hawa kwa uweza wako, kutoka kati yao; 14 kisha watawaambia wenyeji wa nchi hii; wamesikia wao ya kuwa wewe Bwana u kati ya watu hawa; maana, wewe Bwana waonekana uso kwa uso, na wingu lako lasimama juu yao, kisha wewe watangulia mbele yao, katika nguzo ya wingu mchana, na katika nguzo ya moto usiku. 15 Basi kama wewe ukiwaua watu hawa mfano wa mtu mmoja, ndipo mataifa yaliyosikia habari za sifa zako watakaponena na kusema, 16 Ni kwa sababu yeye Bwana hakuweza kuwaleta watu hao kuwatia katika nchi aliyowaapia, kwa ajili ya hayo amewaua nyikani. 17 Basi sasa nakusihi sana, uweza wa Bwana wangu na uwe mkuu, kama ulivyonena, uliposema, 18 Bwana ni mpole wa hasira, mwingi wa rehema, mwenye kusamehe uovu na makosa, naye hatamfanya mwenye hatia kuwa hana makosa kwa njia yo yote; mwenye kuwapatiliza wana kwa uovu wa baba zao, katika kizazi cha tatu na cha nne. 19 Nakusihi, usamehe uovu wa watu hawa, kama ukuu wa rehema yako ulivyo, kama ulivyowasamehe watu hawa, tangu huko Misri hata hivi sasa. 20 Bwana akasema, Mimi nimewasamehe kama neno lako lilivyokuwa; 21 lakini hakika yangu, kama niishivyo, tena kama dunia hii nzima itakavyojawa na utukufu wa Bwana; 22 kwa sababu watu hawa wote, ambao wameuona utukufu wangu na ishara zangu, nilizozitenda huko Misri, na huko jangwani, pamoja na haya wamenijaribu mara hizi kumi, wala hawakuisikiza sauti yangu; 23 hakika yangu hawataiona hiyo nchi niliyowaapia baba zao, wala katika hao wote walionidharau hapana atakayeiona; 24 lakini mtumishi wangu Kalebu, kwa kuwa alikuwa na roho nyingine ndani yake, naye ameniandama kwa moyo wote, nitamleta yeye mpaka nchi hiyo aliyoingia; na uzao wake wataimiliki. 25 Basi Mwamaleki na Mkanaani wakaa katika bonde; kesho geukeni, mkaende jangwani kwa njia iendayo Bahari ya Shamu. 26 Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 27 Je! Nichukuane na mkutano mwovu huu uninung'unikiao hata lini? Nimesikia manung'uniko ya wana wa Israeli, waninung'unikiayo. 28 Waambieni, Kama niishivyo, asema Bwana, hakika yangu kama ninyi mlivyonena masikioni mwangu, ndivyo nitakavyowafanyia ninyi; 29 mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili, na wote waliohesabiwa miongoni mwenu, kama jumla ya hesabu yenu, tangu waliopata umri wa miaka ishirini na zaidi, hao walioninung'unikia, 30 hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni. 31 Lakini Watoto wenu, ambao mlisema watakuwa mateka, ndio nitakaowaleta na kuwatia ndani, nao wataijua nchi ninyi mliyoikataa. 32 Lakini katika habari zenu, mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili. 33 Kisha watoto wenu watakuwa wachungaji jangwani muda wa miaka arobaini nao watauchukua mzigo wa uasherati wenu, hata mizoga yenu itakapoangamia jangwani. 34 Kwa hesabu ya hizo siku mlizoipeleleza ile nchi, yaani, siku arobaini kila siku kuhesabiwa mwaka, mtayachukua maovu yenu, ndiyo miaka arobaini, nanyi mtakujua kufarikana kwangu. 35 Mimi Bwana nimekwisha nena, hakika yangu ndilo nitakaloutenda mkutano mwovu huu wote, waliokusanyika juu yangu; wataangamia katika nyika hii, nako ndiko Watakakokufa. 36 Kisha hao watu, ambao Musa aliwatuma waipeleleze nchi, waliorudi, na kufanya mkutano wote kumnung'unikia, kwa walivyoleta habari mbaya juu ya nchi, 37 watu hao walioileta habari mbaya ya nchi wakafa kwa tauni mbele ya Bwana. 38 Lakini Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, wakabaki hai miongoni mwa wale watu waliokwenda kuipeleleza nchi. 39 Kisha Musa akawaambia wana wa Israeli wote maneno haya, na hao watu wakaombolea sana. 40 Wakainuka na mapema asubuhi, wakakwea juu ya mlima hata kileleni, wakisema, Tazameni, sisi tupo hapa, nasi tutakwea kwenda mahali Bwana alipotuahidi; kwani tumefanya dhambi. 41 Musa akawaambia, Kwa nini ninyi sasa kuyahalifu maagizo ya Bwana? Maana halitafanikiwa jambo hilo. 42 Msikwee, kwa kuwa Bwana hamo kati yenu; msipigwe na kuangushwa mbele ya adui zenu. 43 Kwa kuwa Mwamaleki na Mkanaani wako mbele yenu, nanyi mtaanguka kwa upanga, kwa sababu mmerudi nyuma msimwandame Bwana, kwa hiyo Bwana hatakuwa pamoja nanyi. 44 Lakini walithubutu kukwea mlimani hata kileleni; ila sanduku la agano la Bwana halikutoka humo maragoni, wala Musa hakutoka. 45 Ndipo Mwamaleki, na Mkanaani waliokaa huko mlimani, wakatelemka, wakawapiga na kuwaangusha, hata kufikilia Horma.

Hesabu 15

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Nena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Mtakapoingia nchi yenu ya kukaa, niwapayo, 3 nanyi mwataka kumsongezea Bwana sadaka kwa moto, kwamba ni sadaka ya kuteketezwa, au dhabihu ya kuchinjwa, ili kuondoa nadhiri, au kuwa sadaka ya hiari, au katika sikukuu zenu zilizoamriwa, ili kumfanyia Bwana harufu ipendezayo, katika ng'ombe, au katika kondoo; 4 ndipo yeye atakayetoa matoleo yake na amtolee Bwana sadaka ya unga ya sehemu ya kumi ya efa ya unga mwembamba uliochanganywa na robo ya hini ya mafuta; 5 na divai kwa sadaka ya kinywaji, robo ya hini, utaiandaa pamoja na sadaka ya kuteketezwa, au kwa dhabihu ya kuchinjwa, kwa ajili ya kila mwana-kondoo. 6 Au kwa ajili ya kondoo mume, utaiandaa sadaka ya unga ya sehemu za kumi mbili za efa ya unga mwembamba uliochanganywa na sehemu ya tatu ya hini ya mafuta; 7 na kwa sadaka ya kinywaji utasongeza sehemu ya tatu ya hini ya divai, kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana. 8 Tena hapo utakapomwandaa ng'ombe mume kwa sadaka ya kuteketezwa, au kwa dhabihu ya kuchinjwa, kwa kuondoa nadhiri, au kwa sadaka za amani kwa Bwana; 9 ndipo utakapotoa, pamoja na huyo ng'ombe, sadaka ya unga ya sehemu za kumi tatu za efa ya unga mwembamba uliochanganywa na nusu ya hini ya mafuta. 10 Tena utasongeza nusu ya hini ya divai kwa sadaka ya kinywaji, kwa sadaka iliyosongezwa kwa moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana. 11 Ndivyo itakavyofanywa kwa kila ng'ombe, au kwa kila kondoo mume, au kwa kila mwana-kondoo mume, au kila mwana-mbuzi. 12 Kama hesabu ilivyo ya hao mtakaowaandaa, ndivyo mtakavyofanya kwa kila mmoja, sawasawa na hesabu yao. 13 Wote ambao wamezaliwa kwenu watafanya hayo yote kwa kuandama mfano huo, katika kusongeza sadaka kwa moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana. 14 Tena kwamba mgeni amekaa kwenu, au mtu ye yote aliye kati yenu katika vizazi vyenu, naye yuataka kusongeza sadaka kwa moto, na harufu ya kupendeza kwa Bwana; kama ninyi mfanyavyo, na yeye atafanya vivyo. 15 Katika huo mkutano, kutakuwa na amri moja kwenu ninyi na kwa mgeni akaaye pamoja nanyi; ni amri ya milele katika vizazi vyenu; kama ninyi mlivyo, na mgeni atakuwa vivyo mbele za Bwana. 16 Itakuwa sheria moja na amri moja kwenu ninyi na kwa mgeni akaaye nanyi. 17 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 18 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapoingia nchi niwapelekayo, 19 ndipo itakapokuwa ya kwamba hapo mtakapokula katika chakula cha nchi hiyo, mtamsongezea Bwana sadaka ya kuinuliwa. 20 Katika unga wenu wa kwanza wa chenga-chenga mtasongeza mkate uwe sadaka ya kuinuliwa; vile vile kama mfanyavyo sadaka ya kuinuliwa ya sakafu ya kupuria nafaka, ndivyo mtakavyoiinua. 21 Malimbuko ya unga wenu mtampa Bwana sadaka ya kuinuliwa, katika vizazi vyenu. 22 Tena mtakapokosa, msiyashike maagizo hayo yote Bwana aliyomwambia Musa, 23 hayo yote Bwana aliyowaagiza kwa mkono wa Musa, tangu siku hiyo Bwana aliyoleta maagizo, na baadaye katika vizazi vyenu 24 ndipo itakapokuwa, kama ni kosa lililofanywa pasipo kujua, wala mkutano haukuwa na fahamu, ndipo mkutano wote utasongeza ng'ombe mume mmoja mdogo kuwa sadaka ya kuteketezwa, kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana, pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji, kama amri ilivyo, na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi. 25 Naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya mkutano wote wa wana wa Israeli, nao watasamehewa; maana, lilikuwa ni kosa, nao wamekwisha leta matoleo yao, sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto, na sadaka yao ya dhambi pia wameileta mbele za Bwana kwa ajili ya kosa lao; 26 nao mkutano wote wa wana wa Israeli watasamehewa, na mgeni akaaye kati yao; maana, katika habari za hao wote jambo hilo lilitendeka pasipo kujua. 27 Tena kama mtu mmoja akifanya dhambi pasipo kujua, ndipo atasongeza mbuzi mmoja mke wa mwaka wa kwanza kuwa sadaka ya dhambi. 28 Naye kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya huyo mtu akosaye, atakapofanya dhambi pasipo kujua, mbele za Bwana, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake; naye atasemehewa. 29 Mtakuwa na sheria moja kwa huyo afanyaye neno lo lote pasipo kujua, kwa huyo aliyezaliwa kwenu kati ya wana wa Israeli, na kwa mgeni akaaye kati yao. 30 Lakini mtu afanyaye neno lo lote kwa kusudi, kama ni mzalia, kama ni mgeni, huyo amtukana Bwana; na mtu huyo atakatiliwa mbali na watu wake. 31 Kwa sababu amelidharau neno la Bwana, na kuyavunja maagizo yake; mtu huyo atakatiliwa mbali, uovu wake utakuwa juu yake. 32 Kisha wakati huo wana wa Israeli walipokuwako jangwani, wakamwona mtu mmoja akikusanya kuni siku ya Sabato. 33 Hao waliomwona akikusanya kuni wakamleta kwa Musa na Haruni, na kwa mkutano wote. 34 Nao wakamweka kifungoni, maana, lilikuwa halijasemwa atakalotendwa. 35 Bwana akamwambia Musa, Mtu huyo lazima atauawa; mkutano wote watampiga kwa mawe huko nje ya marago. 36 Basi mkutano wote wakampeleka nje ya marago, nao wakampiga kwa mawe, akafa; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 37 Kisha Bwana akasema na Musa, na kumwambia, 38 Nena na wana wa Israeli, na kuwaagiza ya kwamba wajifanyie vishada katika ncha za nguo zao, katika vizazi vyao, tena ya kwamba watie katika kila kishada cha kila ncha nyuzi za rangi ya samawi; 39 nacho kitakuwa kwenu ni kishada, ili mpate kukiangalia, na kuyakumbuka maagizo yote ya Bwana, na kuyafanya; tena kwamba msiende kutanga-tanga kuandama mioyo yenu wenyewe, na macho yenu wenyewe, ambayo mlikuwa mkiyaandama kwa uasherati hapo kwanza; 40 ili mpate kukumbuka na kuyafanya maagizo yangu yote, na kuwa watakatifu kwa Mungu wenu. 41 Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, niliyewaleta kutoka nchi ya Misri, ili kwamba niwe Mungu wenu; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.

Hesabu 16

1 Basi Kora, mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, akatwaa watu, pamoja na Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni, mwana wa Pelethi, waliokuwa wana wa Reubeni; 2 nao, pamoja na watu kadha wa kadha wa wana wa Israeli, watu mia mbili na hamsini, Wakuu wa mkutano, waliokuwa wateule wa mkutano, watu wenye sifa, wakainuka mbele ya Musa; 3 nao wakakusanyika kinyume cha Musa na Haruni, na kuwaambia, Ninyi inawatosha, kwa kuwa mkutano wote ni mtakatifu, kila mmoja miongoni mwao, Bwana naye yu kati yao; n'nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa Bwana? 4 Musa aliposikia maneno haya, akapomoka kifudifudi; 5 kisha akanena na Kora na mkutano wake wote, akawaambia, Asubuhi Bwana ataonyesha ni kina nani walio wake, kisha ni nani aliye mtakatifu, tena ni nani atakayemkaribisha kwake; maana, yeye atakayemchagua ndiye atakayemsongeza kwake. 6 Fanyeni neno hili; twaeni vyetezo, ninyi Kora na mkutano wake wote; 7 vitieni na moto, mkaweke na uvumba juu yake mbele za Bwana kesho; kisha itakuwa ya kwamba mtu Bwana atakayemchagua, yeye atakuwa mtakatifu; inawatosha ninyi, enyi wana wa Lawi. 8 Musa akamwambia Kora, Sikizeni basi, enyi Wana wa Lawi; 9 Je! Mwaona kuwa ni jambo dogo kwenu, kuwa Mungu wa Israeli amewatenga ninyi na mkutano wa Israeli, ili apate kuwakaribisha kwake; ili mfanye utumishi wa maskani ya Bwana, na kusimama mbele ya mkutano ili kuwatumikia; 10 tena ya kuwa amekuleta uwe karibu, na ndugu zako wote wana wa Lawi pamoja nawe? Nanyi, je! Mwataka na ukuhani pia? 11 Kwa sababu hii wewe na mkutano wako wote mmekusanyika kinyume cha Bwana; na Haruni, je! Yeye ni nani hata mkamnung'unikia? 12 Kisha Musa akatuma kuwaita Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu; nao wakasema, Hatuji sisi; 13 je! Ni jambo dogo, wewe kutuleta kutoka nchi iliyojawa na maziwa na asali, ili kutuua jangwani, lakini pamoja na haya wajikuza mwenyewe uwe mkuu juu yetu kabisa? 14 Kisha, hukutuleta katika nchi iliyojawa na maziwa na asali, wala hukutupa urithi wa mashamba, na mashamba ya mizabibu; je! Unataka kuwatoboa macho watu hawa? Hatuji. 15 Musa akakasirika sana, akamwambia Bwana. Usiikubali sadaka yao; mimi sikutwaa hata punda mmoja kwao, wala sikumwumiza hata mtu mmoja miongoni mwao. 16 Kisha Musa akamwambia Kora, Wewe na mkutano wako wote iweni hapa mbele ya Bwana kesho, wewe, na wao, na Haruni; 17 mkatwae kila mtu chetezo chake, na kutia uvumba juu yake, mkavilete mbele za Bwana, vyetezo mia mbili na hamsini; wewe pia, na Haruni, kila mtu na awe na chetezo chake. 18 Basi wakavitwaa kila mtu chetezo chake, wakatia na moto ndani yake, wakatia na uvumba juu ya moto, na kusimama pale mlangoni pa hema ya kukutania, pamoja na Musa na Haruni. 19 Kisha Kora akakutanisha mkutano wote kinyume chao mlangoni pa hema ya kukutania; na utukufu wa Bwana ukatokea mbele ya mkutano wote. 20 Kisha Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 21 Jitengeni ninyi mkaondoke kati ya mkutano huu, ili nipate kuwaangamiza mara moja. 22 Nao wakapomoka kifudifudi, wakasema, Ee Mungu, Mungu wa roho za wenye mwili wote, je! Mtu mmoja atafanya dhambi, nawe utaukasirikia mkutano wote? 23 Bwana akasema na Musa, na kumwambia, 24 Nena na mkutano, na kuwaambia, Ondokeni ninyi hapo karibu na maskani ya Kora, na Dathani, na Abiramu. 25 Basi Musa akainuka na kuwaendea Dathani na Abiramu; na wazee wa Israeli wakaandamana naye. 26 Akasema na mkutano, na kuwaambia, Nawasihi, ondokeni penye hema za hawa watu waovu, wala msiguse kitu chao cho chote, msiangamizwe katika dhambi zao zote. 27 Basi wakaondoka hapo karibu na maskani ya Kora, na Dathani na Abiramu, pande zote; nao kina Dathani na Abiramu wakatoka nje wakasimama mlangoni mwa hema zao, pamoja na wake zao, na wana wao na watoto wao wadogo. 28 Musa akasema, Kwa jambo hili mtajua ya kwamba Bwana amenituma, ili nifanye kazi hizi zote; kwa kuwa mimi sikuzifanya kwa akili zangu mwenyewe. 29 Kama watu hawa wakifa kifo cha sikuzote, kama watu wote wafavyo, au kama wakipatilizwa kwa mapatilizo ya watu wote; hapo basi Bwana hakunituma mimi. 30 Lakini Bwana akiumba kitu kipya, na hiyo nchi ikifunua kinywa chake na kuwameza, pamoja na wote walio nao, nao washukia shimoni wali hai; ndipo mtatambua ya kwamba watu hawa wamemdharau Bwana 31 Basi ilikuwa, hapo alipokwisha kusema maneno haya yote, nchi iliyokuwa chini yao ikapasuka; 32 nchi ikafunua kinywa chake, na kuwameza, na watu wa nyumba zao na wote walioshikamana na Kora, na vyombo vyao vyote. 33 Basi wao, na wote waliokuwa nao, wakashukia shimoni wali hai; nayo nchi ikawafunika wakaangamia kutoka mle mkutanoni. 34 Nao Israeli wote waliokuwa kando-kando yao wakakimbia kwa ajili ya kilio chao; kwa kuwa walisema, Nchi isije kutumeza na sisi. 35 Kisha moto ukatoka kwa Bwana, ukawateketeza hao watu mia mbili hamsini waliofukiza uvumba. 36 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 37 Mwambie Eleazari mwana wa Haruni kuhani, avitoe vile vyetezo hapo penye moto ukaumwage huo moto kule; kwani ni vitakatifu; 38 vile vyetezo vya hao waliofanya dhambi na kuzihasiri nafsi zao wenyewe, na vifanywe mbao za kufuliwa kuwa kifuniko cha madhabahu; kwa kuwa walivisongeza mbele za Bwana, navyo ni vitakatifu; vitakuwa ishara kwa wana wa Israeli. 39 Basi Eleazari kuhani akavitwaa vile vyetezo vya shaba, vilivyosongezwa na hao walioteketezwa; nao wakavifua viwe kifuniko cha madhabahu; 40 viwe ukumbusho kwa wana wa Israeli, ili mgeni awaye yote asiye wa kizazi cha Haruni, asikaribie kufukiza uvumba mbele za Bwana; asiwe mfano wa Kora, na mkutano wake; kama Bwana alivyonena naye, kwa mkono wa Musa. 41 Lakini siku ya pili yake mkutano wote wa wana wa Israeli wakamnung'unikia Musa, na Haruni, wakasema, Ninyi mmewaua watu wa Bwana. 42 Basi ilikuwa, hapo huo mkutano ulipokuwa umekutanika kinyume cha Musa, na kinyume cha Haruni, wakaangalia upande wa hema ya kukutania; na tazama, hilo wingu likaifunika hema, na utukufu wa Bwana ukaonekana. 43 Na Musa na Haruni wakaenda hapo mbele ya hema ya kukutania. 44 Naye Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 45 Ondokeni kati ya mkutano, ili niwaangamize mara moja. Wao wakapomoka kifudifudi. 46 Musa akamwambia Haruni, Haya, shika chetezo chako, ukatie moto ndani yake, moto wa madhabahuni, kisha utie na uvumba juu ya moto, ukakichukue haraka, wende nacho katika huo mkutano, ukawafanyie upatanisho; kwa kuwa ghadhabu zimetoka kwa Bwana; hiyo tauni imeanza. 47 Basi Haruni akakishika chetezo kama Musa alivyonena, akapiga mbio akaenda katikati ya mkutano; na tazama, tauni ilikuwa imeanza kati ya watu; akatia uvumba juu ya moto na kufanya upatanisho kwa ajili ya hao watu. 48 Akasimama kati ya hao waliokufa na hao waliokuwa wakali hai; tauni ikazuiwa. 49 Basi waliokufa kwa tauni walikuwa kumi na nne elfu na mia saba, zaidi ya hao waliokufa katika jambo la Kora. 50 Haruni akamrudia Musa pale mlangoni pa hema ya kukutania; hiyo tauni ikazuiwa.

Hesabu 17

1 Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia, 2 Nena na wana wa Israeli, kisha upokee kwao fimbo, fimbo moja kwa ajili ya nyumba ya kila baba, katika wakuu wao wote, kama nyumba za baba zao zilivyo, fimbo kumi na mbili; kisha andika jina la kila mtu katika fimbo yake. 3 Na katika fimbo ya Lawi utaliandika jina la Haruni; maana, itakuwa fimbo moja kwa kila kichwa cha nyumba za baba zao. 4 Nawe utaziweka katika hema ya kukutania mbele ya huo ushahidi, hapo nikutanapo pamoja nanyi. 5 Kisha itakuwa, mtu huyo nitakayemchagua, fimbo yake itachipuka; nami nitayakomesha kwangu manung'uniko ya wana wa Israeli, wanung'unikiayo juu yenu. 6 Basi Musa akawaambia wana wa Israeli, ndipo wakuu wao wote wakampa fimbo, fimbo moja kwa kila mkuu, kama nyumba za baba zao zilivyokuwa, fimbo kumi na mbili; na fimbo ya Haruni ilikuwa kati ya fimbo zao. 7 Kisha Musa akaziweka hizo fimbo mbele za Bwana katika hema ya kukutania. 8 Ilikuwa siku ya pili yake, Musa akaingia ndani ya hema ya ushahidi; na tazama, ile fimbo ya Haruni iliyokuwa kwa nyumba ya Lawi ilikuwa imechipuka, imetoa michipukizi, na kuchanua maua; na kuzaa malozi mabivu. 9 Kisha Musa akazileta nje hizo fimbo zote kutoka hapo mbele za Bwana na kuziweka mbele ya wana wa Israeli wote; nao wakaangalia, na kila mtu akaitwaa fimbo yake. 10 Kisha Bwana akamwambia Musa, Irudishe fimbo ya Haruni mbele ya ushahidi, ili itunzwe iwe ishara juu ya hawa wana wa maasi; ili uyakomeshe manung'uniko yao waliyoninung'unikia, ili wasife. 11 Basi Musa akafanya vivyo; kama Bwana alivyomwagiza, ndivyo alivyofanya. 12 Kisha wana wa Israeli wakanena na Musa, na kumwambia, Angalia, sisi twafa, twaangamia, sote twaangamia. 13 Kila mtu akaribiaye, aikaribiaye maskani ya Bwana, hufa; je! Tutakufa pia sote?

Hesabu 18

1 Bwana akamwambia Haruni, Wewe na wanao na nyumba ya baba zako pamoja nawe mtachukua uovu wa patakatifu; wewe na wanao pamoja nawe mtauchukua ukuhani wenu. 2 Na ndugu zako nao, kabila ya Lawi, kabila ya baba yako, uwalete karibu pamoja nawe, ili waungwe nawe, na kukuhudumia; bali wewe na wanao pamoja nawe mtakuwa mbele ya hema ya ushahidi. 3 Nao watashika ulinzi kwa amri yako, na ulinzi wa Hema yote; lakini wasikaribie vyombo vya patakatifu, wala madhabahu, wasife, wao pamoja na ninyi. 4 Nao wataungwa nawe, na kuushika ulinzi wa hema ya kukutania, kwa ajili ya utumishi wote wa hema; na mgeni asiwakaribie ninyi. 5 Nanyi mtashika ulinzi wa patakatifu, na ulinzi wa madhabahu, isiwe ghadhabu juu ya wana wa Israeli tena. 6 Nami, tazama, nimewatwaa ndugu zenu Walawi miongoni mwa wana wa Israeli; kwenu ninyi watu hao ni kipawa alichopewa Bwana, waufanye utumishi wa hema ya kukutania. 7 Nawe na wanao pamoja nawe mtautunza ukuhani wenu, kwa ajili ya kila kitu cha madhabahu, na kwa ajili ya vile vilivyomo ndani ya pazia, nanyi mtatumika. Nawapeni ukuhani kuwa utumishi wa kipawa; na mgeni akaribiaye atauawa. 8 Kisha Bwana akamwambia Haruni, Tazama, nimekupa wewe ulinzi wa sadaka zangu za kuinuliwa, maana, vitu vyote vya hao wana wa Israeli vilivyowekwa wakfu; nimekupa wewe na wanao vitu hivyo kwa ajili ya kule kutiwa mafuta kwenu, kuwa haki yenu milele. 9 Vitu hivi vitakuwa vyako katika vile vilivyo vitakatifu sana, visiteketezwe motoni; matoleo yao yote, maana, kila sadaka yao ya unga, na kila sadaka yao ya dhambi, na kila sadaka yao ya hatia watakayonitolea, vitakuwa vitakatifu sana kwa ajili yako wewe na kwa wanao. 10 Utakula vitu hivyo kuwa ni vitu vitakatifu sana; kila mume atakula vitu hivyo; vitakuwa vitakatifu kwako wewe. 11 Tena kitu hiki ni chako; ile sadaka ya kuinuliwa ya kipawa chao, maana, sadaka za kutikiswa zote za wana wa Israeli; hizi nimekupa wewe, na wanao na binti zako pamoja nawe, ni haki yenu milele; kila mtu katika nyumba yako aliye safi atakula katika hizo. 12 Yaliyo mazuri katika mafuta, na yaliyo mazuri ya mavuno ya zabibu, na ya mavuno ya nafaka, malimbuko yake watakayompa Bwana, amekupa wewe hayo. 13 Matunda ya kwanza yaivayo katika yote yaliyo katika nchi yao, watakayomletea Bwana, yatakuwa yako, kila mtu aliye safi katika nyumba yako atakula katika vitu hivyo. 14 Kila kitu kilichowekwa wakfu katika Israeli kitakuwa chako. 15 Kila kifunguacho tumbo, cha wenye mwili wote watakachomsongezea Bwana cha wanadamu na cha wanyama, ni chako; lakini mzaliwa wa kwanza wa binadamu, huna budi utamkomboa, na mzaliwa wa kwanza wa wanyama wasio safi utamkomboa. 16 Na hao watakaokombolewa katika wanyama hao, tangu aliyepata umri wa mwezi mmoja utamkomboa, kama utakavyohesabu kima chake, kwa fedha ya shekeli tano, kwa shekeli ya mahali patakatifu (nayo ni gera ishirini). 17 Lakini mzaliwa wa kwanza wa ng'ombe, au mzaliwa wa kwanza wa kondoo, au mzaliwa wa kwanza wa mbuzi, hutawakomboa hao; maana, ni watakatifu hao; utanyunyiza damu yao katika madhabahu, na kuyateketeza mafuta yao kuwa sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto, iwe harufu ya kupendeza. 18 Tena nyama yao itakuwa ni yako wewe, kama kile kidari cha kutikiswa, na kama mguu wa nyuma wa upande wa kuume, itakuwa yako. 19 Sadaka zote za kuinuliwa za vitu vitakatifu, wana wa Israeli wavisongezavyo kwa Bwana, nimekupa wewe na wanao na binti zako pamoja nawe, ni haki yenu ya milele; ni agano la chumvi la milele mbele za Bwana kwa ajili yako, na kizazi chako pamoja nawe. 20 Kisha Bwana akamwambia Haruni, Wewe hutakuwa na urithi katika nchi yao, wala hutakuwa na fungu lo lote kati yao; mimi ni fungu lako, na urithi wako, katika wana wa Israeli. 21 Na wana wa Lawi, nimewapa zaka yote katika Israeli kuwa urithi wao, badala ya huo utumishi wautumikao, maana, ni huo utumishi wa hema ya kukutania. 22 Mwanzo wa sasa wana wa Israeli wasikaribie hema ya kukutania, wasije wakachukua dhambi, nao wakafa. 23 Lakini Walawi watatumika utumishi wa hema ya kukutania, nao watauchukua uovu wao; hii itakuwa amri ya milele katika vizazi vyenu vyote, na kati ya wana wa Israeli hawatakuwa na urithi. 24 Kwa kuwa zaka ya wana wa Israeli, waisongezayo kuwa sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana, nimewapa Walawi kuwa urithi wao; kwa hiyo nimewaambia, ya kwamba, katika wana wa Israeli hawatakuwa na urithi uwao wote. 25 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 26 Tena utanena na Walawi, na kuwaambia, Hapo mtakapoitwaa zaka mkononi mwa wana wa Israeli niliyowapa ninyi kutoka kwao kuwa urithi wenu, ndipo mtakaposongeza sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana katika hiyo, iwe zaka katika hiyo zaka. 27 Na sadaka yenu ya kuinuliwa itahesabiwa kwenu, kama ndiyo nafaka ya sakafu ya kupuria, na kama kujaa kwake kinu cha kushindikia zabibu. 28 Hivyo ninyi nanyi mtasongeza sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana katika zaka zenu zote, mpokeazo mikononi mwa wana wa Israeli; kwa hiyo mtampa Haruni kuhani hiyo sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana. 29 Katika vipawa vyenu vyote mtasongeza kila sadaka ya kuinuliwa ya Bwana, ya wema wake wote, hiyo sehemu yake iliyowekwa takatifu. 30 Kwa ajili ya hayo utawaambia, Mtakapoinua humo hayo yaliyo mema, ndipo yatahesabiwa kuwa ya Walawi, kama kuongea kwake sakafu ya kupuria nafaka, na kama maongeo ya kinu cha kushindikia zabibu. 31 Nanyi mtakula hayo kila mahali, ninyi na watu wa nyumbani mwenu; kwa kuwa ni thawabu yenu badala ya utumishi wenu katika hema ya kukutania. 32 Nanyi hamtachukua dhambi kwa ajili yake, hapo mtakapokwisha kuinua humo hayo mema yake; lakini msivitie unajisi vile vitu vitakatifu vya wana wa Israeli, ili msife.

Hesabu 19

1 Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, 2 Hii ndiyo amri ya sheria Bwana aliyoagiza, akisema, Waambie wana wa Israeli wakuletee ng'ombe mke mwekundu asiye na kipaku, mkamilifu, ambaye hajatiwa nira bado; 3 nanyi mtamleta kwa Eleazari kuhani, naye atakwenda naye nje ya kambi, na mtu mmoja atamchinja mbele yake; 4 kisha Eleazari kuhani atatwaa katika damu yake kwa kidole chake, na kuinyunyiza damu yake kuelekea upande wa mbele wa hema ya kukutania mara saba; 5 kisha mtu mmoja atamchoma moto huyo ng'ombe mbele yake; ngozi yake, na nyama yake, na damu yake, pamoja na mavi yake pia atachoma moto; 6 kisha kuhani atatwaa mti wa mwerezi, na hisopo, na sufu nyekundu, na kuvitupa katika huo moto unaomchoma ng'ombe. 7 Ndipo kuhani atazifua nguo zake, na kuoga mwili wake majini, kisha baadaye ataingia kambini, naye kuhani atakuwa najisi hata jioni. 8 Na huyo aliyemchoma moto ng'ombe atazifua nguo zake majini, na kuoga mwili wake majini, naye atakuwa najisi hata jioni. 9 Kisha mtu mmoja aliye safi atayazoa majivu ya huyo ng'ombe, na kuyaweka yawe akiba katika mahali safi nje ya kambi, nayo yatatunzwa kwa ajili ya mkutano wa wana wa israeli, kuwa ndiyo maji ya farakano; ni sadaka ya dhambi. 10 Na yeye ayazoaye majivu ya huyo ng'ombe atazifua nguo zake, naye atakuwa najisi hata jioni; na jambo hili litakuwa amri ya milele, kwa wana wa Israeli, na wa mgeni akaaye kati yao. 11 Mtu agusaye maiti ye yote atakuwa najisi muda wa siku saba; 12 naye atajitakasa kwa yale maji siku ya tatu, na siku ya saba atakuwa safi; lakini kama hajitakasi siku ya tatu, ndipo na siku ya saba hatakuwa safi. 13 Mtu awaye yote agusaye maiti wa mtu aliyekufa, asijitakase, yuatia unajisi maskani ya Bwana; na mtu huyo atakatiliwa mbali na Israeli; maana, hayo maji ya farakano hayakunyunyizwa juu yake, atakuwa najisi; unajisi wake ukali juu yake bado. 14 Hii ndiyo amri, mtu afapo ndani ya hema; kila mtu aingiaye ndani ya hema hiyo, na kila mtu aliye humo hemani, atakuwa najisi muda wa siku saba. 15 Na kila chombo kilicho wazi, kisichofungwa na kifuniko, ni najisi. 16 Kisha mtu ye yote huko nje shambani atakayemgusa mtu aliyeuawa kwa upanga, au mzoga, au mfupa wa mtu, au kaburi, atakuwa najisi muda wa siku saba. 17 Na kwa huyo aliye najisi watatwaa katika majivu ya kuchomwa kwake hiyo sadaka ya dhambi, na maji ya mtoni yatachanganywa na majivu katika chombo; 18 kisha mtu mmoja aliye safi atatwaa hisopo, na kuitia katika hayo maji naye atayanyunyiza juu ya hema, na juu ya vyombo vyote, na juu ya watu waliokuwapo, na juu yake yeye aliyeugusa mfupa, au mtu aliyeuawa, au mzoga, au kaburi; 19 na yule aliye safi atamnyunyiza huyo aliye najisi siku ya tatu, na siku ya saba; na katika siku ya saba atamtakasa; naye atazifua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa safi jioni. 20 Lakini mtu atakayekuwa najisi, naye hataki kujitakasa, mtu huyo atakatiliwa mbali katika mkutano, kwa sababu amepatia unajisi mahali patakatifu pa Bwana; hayo maji ya farakano hayakunyunyizwa juu yake; yeye yu najisi. 21 Nayo itakuwa amri ya sikuzote kwao; na yeye anyunyizaye maji ya farakano atazifua nguo zake; naye ayagusaye hayo maji ya farakano atakuwa najisi hata jioni. 22 Na kitu cho chote atakachokigusa mtu aliye najisi kitakuwa najisi; na mtu atakayekigusa kitu hicho atakuwa najisi hata jioni.

Hesabu 20

1 Kisha wana wa Israeli, mkutano wote, wakaingia bara ya Sini, katika mwezi wa kwanza, watu wakakaa Kadeshi; Miriamu akafa huko, akazikwa huko. 2 Na hapo hapakuwa na maji kwa ule mkutano; wakajikusanya juu ya Musa na juu ya Haruni. 3 Watu wakashindana na Musa, wakanena, wakisema, Ingalikuwa heri kama tungalikufa wakati ule ndugu zetu walipokufa mbele za Bwana! 4 Mbona mmewaleta kusanyiko la Bwana hata jangwa hili ili tufe huku, sisi na wanyama wetu? 5 Na mbona mmetupandisha kutoka Misri ili kutuleta hata mahali hapa pabaya? Si mahali pa mbegu, wala tini, wala mizabibu, wala makomamanga; wala hapana maji ya kunywa. 6 Musa na Haruni wakatoka pale palipokuwa mkutano, wakaenda hata mlangoni pa hema ya kukutania, wakaanguka kifudifudi; utukufu wa Bwana ukawatokea. 7 Bwana akasema na Musa, akinena, 8 Twaa ile fimbo, ukawakusanye mkutano, wewe na Haruni ndugu yako, ukauambie mwamba mbele ya macho yao utoe maji yake, nawe utawatokezea maji katika mwamba, na hivyo utawanywesha maji mkutano na wanyama wao. 9 Musa akaitwaa hiyo fimbo kutoka mbele za Bwana kama alivyomwamuru. 10 Musa na Haruni wakawakusanya kusanyiko mbele ya mwamba, akawaambia, Sikieni sasa, enyi waasi; je! Tuwatokezee maji katika mwamba huu? 11 Musa akainua mkono wake akaupiga ule mwamba kwa fimbo yake mara mbili; maji yakatoka mengi, mkutano wakanywa na wanyama wao pia. 12 Bwana akamwambia Musa na Haruni, Kwa kuwa hamkuniamini mimi, ili kunistahi mbele ya macho ya wana wa Israeli, basi kwa sababu hiyo, hamtawaingiza kusanyiko hili katika ile nchi niliyowapa. 13 Maji haya ni maji ya Meriba; kwa sababu wana wa Israeli waliteta na Bwana, naye alijionyesha kuwa mtakatifu kati yao. 14 Kisha Musa akatuma wajumbe kutoka Kadeshi wamwendee mfalme wa Edomu, na kusema, Ndugu yako Israeli asema, Wewe wazijua taabu zote zilizotupata; 15 jinsi baba zetu walivyotelemkia Misri, nasi tulikaa Misri muda mwingi, nao Wamisri walitutenda vibaya sana, na baba zetu pia; 16 tena tulipomlilia Bwana, akatusikiza sauti yetu, akamtuma malaika, na kututoa tutoke Misri; nasi tupo hapa Kadeshi, mji wa mpakani mwako mwa mwisho; 17 tafadhali utupe ruhusa tupite katika nchi yako; hatutapita katika mashamba, wala katika mashamba ya mizabibu, wala hatutakunywa maji ya visimani; tutaifuata njia kuu ya mfalme, tusigeuke kwenda upande wa kuume, wala upande wa kushoto, hata tutakapopita mpaka wako. 18 Edomu akamwambia, Hutapita katika nchi yangu, nisije nikakutokea kupigana nawe kwa upanga. 19 Wana wa Israeli wakamwambia, Tutakwea kwa njia kuu; tena kama tukinywa maji yako, mimi na wanyama wangu wa mifugo, ndipo nitakulipa thamani yake; nipe ruhusa nipite kwa miguu yangu wala sitaki neno lingine lo lote. 20 Akamwambia, Hutapita katika nchi yangu. Kisha Edomu akamtokea ili kupigana naye, na watu wengi, na kwa mkono wa nguvu. 21 Basi hivyo Edomu akakataa kumpa Israeli ruhusa kupita katika mipaka yake; kwa hivyo Israeli akageuka na kumwacha. 22 Kisha wakasafiri kutoka Kadeshi; wana wa Israeli, mkutano mzima, wakafikilia mlima wa Hori. 23 Bwana akanena na Musa na Haruni katika mlima wa Hori, karibu na mpaka wa nchi ya Edomu, akawaambia, 24 Haruni atakusanywa awe pamoja na watu wake; kwa kuwa hataingia katika nchi niliyowapa wana wa Israeli, kwa sababu mliasi kinyume cha neno langu hapo penye maji ya Meriba. 25 Uwatwae Haruni na mwanawe Eleazari uwalete juu ya mlima wa Hori; 26 umvue Haruni mavazi yake, ukamvike Eleazari mwanawe mavazi hayo; kisha Haruni atakusanywa kwa watu wake, naye atakufa huko. 27 Musa akafanya kama Bwana alivyomwagiza; wakakwea katika mlima wa Hori mbele ya macho ya mkutano wote. 28 Kisha Musa akamvua Haruni mavazi yake, akamvika mwanawe Eleazari mavazi hayo; Haruni akafa huko katika kilele cha mlima; Musa na Eleazari wakatelemka mlimani. 29 Na mkutano wote ulipoona ya kuwa Haruni amekufa, wakamwombolea Haruni muda wa siku thelathini, maana, nyumba yote ya Israeli ikamwombolea.

Hesabu 21

1 Na Mkanaani, mfalme wa Aradi, aliyeketi upande wa Negebu, alisikia habari ya kuwa Israeli alikuja kwa njia ya Atharimu; basi akapigana na Israeli, na watu kadha wa kadha miongoni mwao akawateka mateka. 2 Basi Israeli akaweka nadhiri kwa Bwana akasema, Kama wewe utawatia watu hawa mikononi mwangu kweli ndipo mimi nitaiharibu miji yao kabisa. 3 Bwana akasikiza sauti ya Israeli, akawatia Wakanaani mikononi mwao; nao wakawaharibu wao na miji yao kabisa; na jina la mahali hapo likaitwa Horma. 4 Wakasafiri kutoka mlima wa Hori kwa njia ya Bahari ya Shamu; ili kuizunguka nchi ya Edomu, watu wakafa moyo kwa sababu ya ile njia. 5 Watu wakamnung'unikia Mungu, na Musa, Mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? Maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu. 6 Bwana akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa. 7 Watu wakamwendea Musa, wakasema, Tumefanya dhambi kwa sababu tumemnung'unikia Mungu, na wewe; utuombee kwa Bwana, atuondolee nyoka hawa. Basi Musa akawaombea watu. 8 Bwana akamwambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo ataishi. 9 Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi. 10 Kisha wana wa Israeli wakasafiri, wakapanga marago Obothi. 11 Wakasafiri kutoka Obothi, wakapanga Iye-abarimu, katika jangwa iliyoelekea Moabu, upande wa maawio ya jua. 12 Kutoka huko wakasafiri, wakapanga katika bonde la Zeredi. 13 Kutoka huko wakasafiri, wakapanga upande wa pili wa Arnoni, ulio jangwani, utokao katika mpaka wa Waamori; maana, Arnoni ndio mpaka wa Moabu, kati ya Moabu na Waamori. 14 Kwa hiyo imesemwa katika chuo cha Vita vya Bwana, Wahebu katika Sufa, Na bonde za Arnoni, 15 Na matelemko ya hizo bonde Kwenye kutelemkia maskani ya Ari, Na kutegemea mpaka wa Moabu. 16 Kutoka huko wakasafiri kwenda Beeri; ni kisima ambacho Bwana alimwambia Musa, Uwakutanishe watu, nami nitawapa maji. 17 Ndipo Israeli wakaimba wimbo huu; Bubujika Ee kisima; kiimbieni; 18 Kisima walichokichimba wakuu, Ambacho wakuu wa watu wakakifukua, Kwa fimbo za enzi, kwa fimbo zao. 19 na kutoka Matana wakaenda Nahalieli; na kutoka Nahalieli wakaenda Bamothi; 20 na kutoka Bamothi wakaenda bondeni kwenye konde la Moabu, hata kilele cha Pisga, kielekeacho chini jangwani. 21 Kisha Israeli akatuma wajumbe kumwendea Sihoni mfalme wa Waamori, na kusema, 22 Nipe ruhusa nipite katika nchi yako; hatutageuka kando kwenda mashambani, wala kuingia katika mashamba ya mizabibu hatutakunywa maji ya visimani; tutakwenda kwa njia kuu ya mfalme, hata tutakapokuwa tumepita mpaka wako. 23 Lakini Sihoni hakukubali kumwacha Israeli kupita katika mpaka wake; bali Sihoni akawakutanisha watu wake wote, akatoka aende kupigana na Israeli jangwani, akafika mpaka Yahasa; akapigana na Israeli. 24 Israeli wakampiga kwa makali ya upanga, na kuimiliki nchi yake, tangu mto wa Arnoni hata mto wa Yaboki, mpaka nchi ya wana wa Amoni; kwa kuwa mpaka wa wana wa Amoni ulikuwa una nguvu. 25 Basi Israeli wakaitwaa miji hiyo yote; Israeli wakakaa katika miji yote ya Waamori, katika Heshboni, na miji yake yote. 26 Kwa kuwa Heshboni ulikuwa ni mji wa Sihoni mfalme wa Waamori, aliyekuwa akipigana na mfalme wa Moabu wa mbele, na kumpokonya nchi yake yote mkononi mwake, mpaka mto wa Arnoni. 27 Kwa hiyo, hao wanenao kwa mithali wasema, Njoni Heshboni, Mji wa Sihoni na ujengwe na kuthibitishwa; 28 Maana, moto umetoka Heshboni, Umekuwa Ari ya Moabu, Mwali wa moto umetoka mji wa Sihoni; Wakuu wa mahali palipoinuka Arnoni 29 Ole wako Moabu! Umeangamia, enyi watu wa Kemoshi; Amewatoa wanawe kuwa wakimbizi, Na binti zake waende utumwani, Wamwendee Sihoni mfalme wa Waamori. 30 Tumewapigia mishale; Heshboni umepotea mpaka Diboni, Nasi tumeharibu mpaka Nofa, Ifikiliayo Medeba. 31 Basi hivyo Israeli akaketi katika nchi ya Waamori. 32 Kisha Musa akapeleka watu ili kupeleleza Yazeri, nao wakaitwaa miji yake, wakawafukuza Waamori waliokuwamo. 33 Kisha wakageuka na kukwea kwa njia ya Bashani; na Ogu mfalme wa Bashani akaondoka apigane nao huko Edrei, yeye na watu wake wote. 34 Bwana akamwambia Musa, Usimche; kwa kuwa nimekwisha mtia mkononi mwako, na watu wake wote, na nchi yake; nawe utamtenda kama ulivyomtenda Sihoni mfalme wa Waamori, aliyeketi Heshboni. 35 Basi wakampiga, na wanawe, na watu wake wote, hata wasisaze kwake mtu ye yote; nao wakaimiliki nchi yake.

Hesabu 22

1 Kisha wana wa Israeli wakasafiri na kupanga katika nchi tambarare za Moabu ng'ambo ya pili ya Yordani karibu ya Yeriko. 2 Na Balaki mwana wa Sipori akaona mambo yote ambayo Israeli wamewatendea Waamori. 3 Moabu akawaogopa hao watu sana, kwa kuwa walikuwa wengi; Moabu akafadhaika kwa sababu ya wana wa Israeli. 4 Moabu akawaambia wazee wa Midiani, Sasa jeshi hili la watu litaramba vitu vyote vinavyotuzunguka, kama vile ng'ombe arambavyo majani ya mashamba. Na Balaki, mwana wa Sipori, alikuwa mfalme wa Moabu zamani zile. 5 Basi akatuma wajumbe kwa Balaamu mwana wa Beori, hata Pethori, ulio kando ya Mto, mpaka nchi ya wana wa watu wake, kwenda kumwita, akisema, Tazama, kuna watu waliotoka Misri; tazama, wanaufunika uso wa nchi, tena wanakaa kunikabili mimi. 6 Basi, njoo wewe, nakusihi unilaanie watu hawa; maana wana nguvu kunishinda mimi. Labda nitawaweza, tupate kuwapiga, niwafukuze watoke katika nchi yangu, kwa maana najua ya kuwa yeye umbarikiye hubarikiwa, na yeye umlaaniye hulaaniwa. 7 Wazee wa Moabu, na wazee wa Midiani, wakaenda, wakichukua ujira wa uganga mikononi mwao; wakamfikilia Balaamu, wakamwambia maneno ya Balaki. 8 Akawaambia, Kaeni hapa usiku huu, nami nitawaletea jawabu kama Bwana atakavyoniambia; wakuu wa Moabu wakakaa na Balaamu. 9 Mungu akamjia Balaamu, akasema, Ni watu gani hawa ulio nao pamoja nawe? 10 Balaamu akamwambia Mungu, Balaki mwana wa Sipori, mfalme wa Moabu, amewatuma kwangu, akisema, 11 Tazama, kuna watu waliotoka Misri, wanaufunika uso wa nchi; basi njoo unilaanie watu hawa; labda nitaweza kupigana nao, na kuwafukuza. 12 Mungu akamwambia Balaamu, Usiende pamoja nao; wala usiwalaani watu hawa, maana wamebarikiwa. 13 Balaamu akaondoka asubuhi akawaambia wakuu wa Balaki, Enendeni zenu hata nchi yenu; kwa maana Bwana amekataa kunipa ruhusa niende pamoja nanyi. 14 Wakuu wakaondoka wakaenda kwa Balaki, wakasema, Balaamu, anakataa kuja pamoja nasi. 15 Basi Balaki akatuma wakuu mara ya pili, wengi zaidi, wenye cheo wakubwa kuliko wale wa kwanza. 16 Wakamfikilia Balaamu, wakamwambia, Balaki mwana wa Sipori asema hivi, Nakusihi, neno lo lote lisikuzuie usinijie; 17 maana nitakufanyizia heshima nyingi sana, na neno lo lote utakaloniomba nitalitenda; basi njoo, nakusihi, unilaanie watu hawa. 18 Balaamu akajibu akawaambia watumishi wa Balaki, Kama Balaki angenipa nyumba yake imejaa fedha na dhahabu, siwezi kupita mpaka wa neno la Bwana, Mungu wangu, kulipunguza au kuliongeza. 19 Basi sasa nawasihi, kaeni hapa tena usiku huu, nipate kujua Bwana atakaloniambia zaidi. 20 Mungu akamjia Balaamu usiku, akamwambia, Kwa kuwa watu hawa wamekuja kukuita, enenda pamoja nao; lakini neno lile nitakalokuambia ndilo utakalolitenda, basi. 21 Balaamu akaondoka asubuhi, akatandika punda wake, akaenda pamoja na wakuu wa Moabu. 22 Hasira ya Mungu ikawaka kwa sababu alikwenda; malaika wa Bwana akajiweka njiani, ili kumpinga. Basi alikuwa amepanda punda wake, na watumishi wake wawili walikuwa pamoja naye. 23 Na yule punda akamwona malaika wa Bwana amesimama njiani, na upanga wake mkononi mwake amekwisha kuufuta; punda akageuka upande ili kuiacha njia, akaingia shambani. Balaamu akampiga punda ili kumrejeza njiani. 24 Kisha malaika wa Bwana akasimama mahali penye bonde, katikati ya mashamba ya mizabibu, tena penye kitalu upande huu na kitalu upande huu. 25 Yule punda akamwona malaika wa Bwana, akajisonga ukutani, akamseta Balaamu mguu wake, basi akampiga mara ya pili. 26 Malaika wa Bwana akaendelea mbele akasimama mahali pembamba sana, hapakuwa na nafasi ya kugeukia mkono wa kuume, wala mkono wa kushoto. 27 Yule punda akamwona malaika wa Bwana, akajilaza chini ya Balaamu; hasira yake Balaamu ikawaka, akampiga punda kwa fimbo yake. 28 Bwana akakifunua kinywa cha yule punda, naye akamwambia Balaamu, Nimekutenda nini, hata ukanipiga mara tatu hizi? 29 Balaamu akamwambia punda; Kwa sababu umenidhihaki; laiti ningekuwa na upanga mkononi mwangu ningekuua sasa hivi. 30 Yule punda akamwambia Balaamu, Je! Mimi si punda wako, nawe umenipanda maisha yako yote hata leo? Nimezoea kukutenda hayo? Akasema, La! 31 Ndipo Bwana akafunua macho ya Balaamu akamwona malaika wa Bwana amesimama njiani, ana upanga mkononi mwake, umekwisha kufutwa naye akainama kichwa, akaanguka kifudifudi. 32 Malaika wa Bwana akamwambia, Mbona umempiga punda wako mara tatu hizi? Tazama mimi nimekuja ili kukupinga, kwa sababu njia yako imepotoka mbele zangu, 33 punda akaniona, akageuka upande mbele zangu mara tatu hizi; kama asingejiepusha nami, bila shaka ningalikuua wewe, nikamwacha yeye hai. 34 Balaamu akamwambia malaika wa Bwana, Nimefanya dhambi; maana sikujua ya kuwa wewe umesimama njiani ili kunipinga; basi sasa, ikiwa umechukizwa, nitarudi tena. 35 Malaika wa Bwana akamwambia Balaamu Enenda pamoja na watu hawa, lakini neno lile nitakalokuambia, ndilo utakalosema. Basi Balaamu akaenda pamoja na wakuu wa Balaki. 36 Balaki aliposikia ya kuwa Balaamu amefika, akatoka kwenda kumlaki, mpaka Mji wa Moabu, ulioko katika mpaka wa Arnoni, ulioko katika upande wa mwisho wa mpaka huo. 37 Balaki akamwambia Balaamu, Je! Mimi sikutuma watu kwako kwa bidii ili kukuita? Mbona hukunijia? Je! Siwezi mimi kukufanyizia heshima nyingi? 38 Balaamu akamwambia Balaki, Tazama, nimekujia. Je! Mimi sasa nina uwezo wo wote kusema neno lo lote? Neno lile Mungu atakalolitia kinywani mwangu, ndilo nitakalolisema. 39 Balaamu akaenda pamoja na Balaki wakafika Kiriath-husothi. 40 Balaki akachinja ng'ombe, na kondoo, akampelekea Balaamu na wale wakuu waliokuwa pamoja naye. 41 Ikawa asubuhi Balaki akamchukua Balaamu, akampandisha hata mahali pa juu pa Baali; na kutoka huko akawaona watu, hata pande zao za mwisho.

Hesabu 23

1 Balaamu akamwambia Balaki, Nijengee hapa madhabahu saba, ukaniandalie hapa ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba. 2 Balaki akafanya kama Balaamu alivyonena. Balaki na Balaamu wakatoa sadaka, ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. 3 Balaamu akamwambia Balaki, Simama karibu na sadaka yako, nami nitakwenda, labda Bwana atakuja kuonana nami; na lo lote atakalonionyesha nitakuambia. Akaenda hata mahali peupe juu ya kilima. 4 Mungu akakutana na Balaamu; naye Balaamu akamwambia, Nimetengeneza madhabahu saba, nami nimetoa sadaka ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. 5 Bwana akatia neno katika kinywa chake Balaamu, akasema, Umrudie Balaki; ukaseme maneno haya. 6 Akarudi kwake, na tazama, amesimama karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, yeye na wakuu wote wa Moabu pamoja naye. 7 Akatunga mithali yake, akasema, Balaki amenileta kutoka Aramu, Mfalme wa Moabu kutoka milima ya mashariki, Njoo! Unilaanie Yakobo, Njoo! Unishutumie Israeli. 8 Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani? Nimshutumuje, yeye ambaye Bwana hakumshutumu? 9 Kutoka kilele cha majabali namwona; Na kutoka milimani namtazama; Angalia, ni watu wakaao peke yao, Wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa. 10 Ni nani awezaye kufanya idadi ya mavumbi ya Yakobo, Au kuhesabu robo ya Israeli? Na nife kifo chake mwenye haki, Na mwisho wangu uwe mfano wa mwisho wake. 11 Balaki akamwambia Balaamu, Umenitendea nini? Nimekuleta ili Uwalaani adui zangu, na tazama, umewabariki kabisa kabisa. 12 Naye akajibu, akasema, Je! Hainipasi kuangalia, niseme neno lile Bwana atialo kinywani mwangu? 13 Balaki akamwambia, Haya! Njoo, tafadhali, hata mahali pengine, na kutoka huko utaweza kuwaona; utaona upande wa mwisho wao tu, wala hutawaona wote, ukanilaanie hao kutoka huko. 14 Akamchukua mpaka shamba la Sofimu, hata kilele cha Pisga, akajenga madhabahu saba, akatoa sadaka ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. 15 Akamwambia Balaki, Simama hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa, nami nitaonana na Bwana kule. 16 Bwana akaonana na Balaamu akatia neno kinywani mwake, akasema, Umrudie Balaki, ukaseme hivi. 17 Akafika kwake, na tazama, amesimama karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, na wakuu wa Moabu pamoja naye. Balaki akamwambia, Bwana amenena nini? 18 Naye akatunga mithali yake, akasema, Ondoka Balaki, ukasikilize; Nisikilize, Ee mwana wa Sipori; 19 Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? 20 Tazama, nimepewa amri kubariki, Yeye amebariki, nami siwezi kulitangua. 21 Hakutazama uovu katika Yakobo, Wala hakuona ukaidi katika Israeli. Bwana, Mungu wake, yu pamoja naye, Na sauti kuu ya mfalme i katikati yao. 22 Mungu amewaleta kutoka Misri, Naye ana nguvu kama nguvu za nyati. 23 Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo, Wala hapana uganga juu ya Israeli. Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa, Ni mambo gani aliyoyatenda Mungu! 24 Tazama, watu hawa wanaondoka kama simba mke, Na kama simba anajiinua nafsi yake, Hatalala hata atakapokula mawindo, Na kunywa damu yao waliouawa. 25 Balaki akamwambia Balaamu, Basi usiwalaani kabisa, wala usiwabariki kabisa. 26 Lakini Balaamu akajibu akamwambia Balaki, Je! Sikukuambia ya kwamba, Kila neno Bwana atakalolisema sina budi kulitenda? 27 Kisha Balaki akamwambia Balaamu, Haya, njoo sasa, nikupeleke mahali pengine; labda Mungu ataridhia kwamba unilaanie watu hao huko. 28 Basi Balaki akamchukua Balaamu akaenda naye mpaka kilele cha mlima Peori, mahali paelekeapo upande wa nyika iliyo chini yake. 29 Balaamu akamwambia Balaki, Haya, unijengee hapa madhabahu saba, kisha uniandalie ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba. 30 Basi Balaki akafanya kama Balaamu alivyosema, akasongeza sadaka ng'ombe mume na kondoo mume juu ya kila madhabahu.

Hesabu 24

1 Basi Balaamu alipoona ya kuwa ilimpendeza Bwana kuwabariki Israeli, hakwenda, kama hapo kwanza, ili kutafuta uchawi, bali alielekeza uso wake jangwani. 2 Balaamu akainua macho yake akawaona Israeli wamekaa kabila kabila; roho ya Mungu ikamjia. 3 Akatunga mithali yake, akasema, Balaamu mwana wa Beori asema, Yule mtu aliyefumbwa macho asema; 4 Asema, yeye asikiaye maneno ya Mungu, Yeye aonaye maono ya Mwenyezi, Akianguka kifudifudi, amefumbuliwa macho; 5 Mahema yako ni mazuri namna gani, Ee Yakobo, Maskani zako, Ee Israeli! 6 Mfano wa bonde zimetandwa, Mfano wa bustani kando ya mto, Mfano wa mishubiri aliyoipanda Bwana, Mfano wa mierezi kando ya maji. 7 Maji yatafurika katika ndoo zake, Na mbegu zake zitakuwa katika maji mengi. Na mfalme wake ataadhimishwa kuliko Agagi, Na ufalme wake utatukuzwa. 8 Mungu amemleta kutoka Misri, Ana nguvu mfano wa nguvu za nyati; Atawameza mataifa walio adui zake, Ataivunja mifupa yao vipande vipande. Atawachoma kwa mishale yake. 9 Aliinama, akalala mfano wa simba, Na kama simba mke; ni nani atakayemstusha? Na abarikiwe kila akubarikiye, Na alaaniwe kila akulaaniye. 10 Hasira ya Balaki ikawaka juu ya Balaamu akayapiga makofi; Balaki akamwambia Balaamu, Nalikuita ili unilaanie adui zangu, na tazama, umewabariki kabisa mara tatu hizi. 11 Basi sasa kimbilia mahali pako; naliazimu kukuheshimu sana; lakini, tazama, Bwana amekuzuilia heshima. 12 Balaamu akamwambia Balaki, Je! Sikuwaambia wajumbe wako ulionipelekea, nikisema, 13 Kama Balaki angenipa nyumba yake imejaa fedha na dhahabu, siwezi kupita mpaka wa neno la Bwana, kutenda neno jema, wala neno baya, kwa nia yangu mwenyewe; Bwana atakalolinena ndilo nitakalolinena mimi. 14 Basi sasa, tazama, ninakwenda kwa watu wangu; haya, nitakuarifu mambo ambayo watu hawa watakayowatenda watu wako siku za mwisho. 15 Akatunga mithali yake akasema, Balaamu mwana wa Beori asema, Yule mtu aliyefumbwa macho asema, 16 Asema, yeye asikiaye maneno ya Mungu, Na kuyajua maarifa yake Aliye Juu. Yeye aonaye maono ya Mwenyezi, Akianguka kifudifudi, amefumbuliwa macho, 17 Namwona, lakini si sasa; Namtazama, lakini si karibu; Nyota itatokea katika Yakobo Na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli; Nayo itazipiga-piga pembe za Moabu, Na kuwavunja-vunja wana wote wa ghasia. 18 Na Edomu itakuwa milki Seiri pia itakuwa milki, waliokuwa adui zake; Israeli watakapotenda kwa ushujaa. 19 Mwenye kutawala atakuja toka Yakobo, Atawaangamiza watakaobaki mjini. 20 Kisha akamwangalia Amaleki, akatunga mithali yake, akasema, Amaleki alikuwa ni wa kwanza wa mataifa; Lakini mwisho wake atafikilia uharibifu. 21 Kisha akamwangalia Mkeni, akatunga mithali yake, akasema, Makao yako yana nguvu, Na kitundu chako kimewekwa katika jabali. 22 Pamoja na haya Wakeni wataangamizwa, Hata Ashuru atakapokuchukua mateka. 23 Akatunga mithali yake akasema, Ole wao! Ni nani atakayepona, Mungu atakapofanya haya? 24 Lakini merikebu zitakuja kutoka pwani kwa Kitimu, Nazo zitamtaabisha Ashuru, na Eberi zitamtaabisha, Yeye naye atafikilia uharibifu. 25 Basi Balaamu akainuka, akaondoka na kurudi mahali pake; Balaki naye akaenda zake.

Hesabu 25

1 Basi Israeli akakaa Shitimu, kisha watu wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu; 2 kwa kuwa waliwaalika hao watu waende sadakani, sadaka walizowachinjia miungu yao; watu wakala chakula, wakaisujudu hiyo miungu yao. 3 Ikawa Israeli kujiungamanisha na Baal-peori; hasira za Bwana zikawaka juu ya Israeli. 4 Kisha Bwana akamwambia Musa, Watwae wakuu wote wa hao watu, ukamtungikie Bwana watu hao mbele ya jua, ili kwamba hizo hasira kali za Bwana ziwaondokee Israeli. 5 Basi Musa akawaambia waamuzi wa Israeli, Waueni kila mtu watu wake waliojiungamanisha na Baal-peori. 6 Na tazama, mtu mmoja miongoni mwa wana wa Israeli akaja na kuwaletea nduguze mwanamke Mmidiani mbele ya macho ya Musa, na mbele ya macho ya mkutano wote wa wana wa Israeli, hapo walipokuwa walia mbele ya mlango wa hema ya kukutania. 7 Naye Finehasi mwana wa Eleazari, mwana wa Haruni kuhani, alipoona jambo hilo, akaondoka hapo katikati ya mkutano, akashika fumo mkononi mwake; 8 akamwandama huyo mtu wa Israeli na kuingia ndani ya hema nyuma yake, naye akawachoma wote wawili kwa fumo lake, yule mume wa Israeli na huyo mwanamke kati ya tumbo lake. Basi pigo likazuiwa kwao wana wa Israeli. 9 Nao waliokufa kwa hilo pigo walikuwa watu elfu ishirini na nne hesabu yao. 10 Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia, 11 Finehasi, mwana wa Eleazari, mwana wa Haruni kuhani, amezigeuza hasira zangu zisiwe juu ya wana Wa Israeli, kwa kuwa alikuwa na wivu kati yao kwa wivu wangu mimi, hata nisiwaangamize wana wa Israeli katika wivu wangu. 12 Basi kwa hiyo, sema, Tazama, nampa yeye agano langu la amani; 13 tena kwake yeye, na kizazi chake baada yake, litakuwa agano la ukuhani wa milele; kwa sababu alikuwa na wivu kwa ajili ya Mungu wake, na kuwafanyia upatanisho wana wa Israeli. 14 Basi jina la Mwisraeli huyo aliyeuawa pamoja na yule mwanamke Mmidiani, aliitwa Zimri, mwana wa Salu, mkuu wa nyumba ya baba zake, katika kabila la Simeoni. 15 Na jina la huyo mwanamke Mmidiani aliyeuawa, aliitwa Kozbi, binti Suri; naye alikuwa kichwa cha watu wa nyumba ya baba zake huko Midiani 16 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 17 Wasumbue Wamidiani, na kuwapiga; 18 kwa sababu wao wawasumbua ninyi kwa hila zao, ambazo kwa hizo wamewadanganya ninyi katika jambo la Peori, na katika jambo la huyo Kozbi, binti wa mkuu wa Midiani, umbu lao, huyo aliyeuawa siku hiyo ya pigo katika jambo la Peori.

Hesabu 26

1 Ikawa baada ya hilo pigo, Bwana akanena na Musa na Eleazari, mwana wa Haruni kuhani, na kuwaambia, 2 Fanya jumla ya mkutano wote wa wana wa Israeli, tangu umri wa miaka ishirini, na zaidi, kwa nyumba za baba zao, hao wote katika Israeli wawezao kutoka kuenenda vitani. 3 Kisha Musa na Eleazari kuhani wakanena nao katika nchi tambarare za Moabu karibu na mto wa Yordani, huko Yeriko, wakawaambia, 4 Fanyeni jumla ya watu, tangu umri wa miaka ishirini, na zaidi; kama Bwana alivyomwagiza Musa na wana wa Israeli, hao waliotoka nchi ya Misri. 5 Reubeni mzaliwa wa kwanza wa Israeli, wana wa Reubeni; wa Hanoki, jamaa ya Wahanoki; na wa Palu, jamaa ya Wapalu; 6 na wa Hesroni, jamaa ya Wahesroni; na wa Karmi, jamaa ya Wakarmi. 7 Hizi ndizo jamaa za Wareubeni; na hao waliohesabiwa kwao walikuwa arobaini na tatu elfu na mia saba na thelathini. 8 Na wana wa Palu; Eliabu. 9 Na wana wa Eliabu; Nemueli, na Dathani, na Abiramu. Hawa ndio Dathani na Abiramu waliochaguliwa na mkutano, ambao walishindana na Musa na Haruni katika mkutano wa Kora, hapo waliposhindana na Bwana; 10 nchi ikafunua kinywa chake, na kuwameza pamoja na Kora, mkutano huo ulipokufa; wakati moto ulipowateketeza watu mia mbili na hamsini, nao wakawa ishara. 11 Pamoja na hayo, hao wana wa Kora hawakufa. 12 Na wana wa Simeoni kwa jamaa zao; wa Yemueli, jamaa ya Wayemueli; wa Yamini, jamaa ya Wayamini; na Yakini, jamaa ya Wayakini; 13 wa Sohari, jamaa ya Wasohari; wa Shauli, jamaa ya Washauli. 14 Hizi ndizo jamaa za Wasimeoni, watu ishirini na mbili elfu na mia mbili. 15 Na wana wa Gadi kwa jamaa zao; wa Sifoni, jamaa ya Wasifoni; wa Hagi, jamaa ya Wahagi; wa Shuni, jamaa ya Washuni; 16 wa Ezboni, jamaa ya Waezboni; wa Eri, jamaa ya Waeri; 17 wa Arodi, jamaa ya Waarodi; wa Areli, jamaa ya Waareli. 18 Hizi ndizo jamaa za wana wa Gadi kama waliohesabiwa kwao, arobaini elfu na mia tano. 19 Na wana wa Yuda, Eri na Onani; na hao Eri na Onani wakafa katika nchi ya Kanaani. 20 Na wana wa Yuda kwa jamaa zao; wa Shela, jamaa ya Washela; wa Peresi, jamaa ya Waperesi; wa Zera, jamaa ya Wazera. 21 Na wana wa Peresi walikuwa; wa Hesroni, jamaa ya Wahesroni; wa Hamuli, jamaa ya Wahamuli. 22 Hizi ndizo jamaa za Yuda kama waliohesabiwa kwao, sabini na sita elfu na mia tano. 23 Na wana wa Isakari kwa jamaa zao; wa Tola, jamaa ya Watola; wa Puva, jamaa ya Wapuva; 24 wa Yashubu, jamaa ya Wayashubu; wa Shimroni, jamaa ya Washimroni. 25 Hizi ndizo jamaa za Isakari kama waliohesabiwa kwao, sitini na nne elfu na mia tatu. 26 Na wana wa Zabuloni kwa jamaa zao; wa Seredi, jamaa ya Waseredi; wa Eloni, jamaa ya Waeloni; wa Yaleeli, jamaa ya Wayaleeli. 27 Hizi ndizo jamaa za Wazabuloni kama waliohesabiwa kwao, sitini elfu na mia tano. 28 Na wana wa Yusufu kwa jamaa zao; Manase na Efraimu. 29 Wana wa Manase; wa Makiri, jamaa ya Wamakiri; na Makiri akamzaa Gileadi; wa Gileadi, jamaa ya Wagileadi. 30 Hawa ndio wana wa Gileadi; wa Abiezeri, jamaa ya Waabiezeri; wa Heleki, jamaa ya Waheleki; 31 na wa Asrieli, jamaa ya Waasrieli; na wa Shekemu, jamaa ya Washekemu; 32 na wa Shemida, jamaa ya Washemida; na wa Heferi, jamaa ya Waheferi. 33 Na Selofehadi mwana wa Heferi hakuwa na wana waume, isipokuwa wa kike; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya, Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. 34 Hizi ndizo jamaa za Manase; na waliohesabiwa kwao walikuwa ni hamsini na mbili elfu na mia saba. 35 Na wana wa Efraimu kwa jamaa zao; wa Shuthela, jamaa ya Washuthela; wa Beredi, jamaa ya Waberedi; wa Tahathi, jamaa ya Watahathi. 36 Na wana wa Shuthela ni hawa; wa Erani, jamaa ya Waerani. 37 Hizi ndizo jamaa za wana wa Efraimu kama waliohesabiwa kwao, thelathini na mbili elfu na mia tano. Hao ndio wana wa Yusufu kwa jamaa zao. 38 Na wana wa Benyamini kwa jamaa zao; wa Bela, jamaa ya Wabela; na wa Ashbeli, jamaa ya Waashbeli; wa Ahiramu, jamaa ya Waahiramu; 39 wa Shufamu, jamaa ya Washufamu; wa Hufamu, jamaa ya Wahufamu. 40 Na wana wa Bela walikuwa Ardi na Naamani; wa Ardi, jamaa ya Waardi; wa Naamani, jamaa ya Wanaamani. 41 Hao ndio wana wa Benyamini kwa jamaa zao; na waliohesabiwa kwao walikuwa arobaini na tano elfu na mia sita. 42 Na wana wa Dani ni hawa kwa jamaa zao; wa Shuhamu, jamaa ya Washuhamu. Hizi ndizo jamaa za Dani kwa jamaa zao. 43 Jamaa zote za Washuhamu, kama waliohesabiwa kwao, walikuwa sitini na nne elfu na mia nne. 44 Na wana wa Asheri kwa jamaa zao; wa Imna, jamaa ya Waimna; wa Ishvi jamaa ya Waishvi; wa Beria, jamaa ya Waberia. 45 Wa wana wa Beria; wa Heberi, jamaa ya Waheberi; wa Malkieli, jamaa ya Wamalkieli. 46 Na jina la binti wa Asheri aliitwa Sera. 47 Hizi ndizo jamaa za wana wa Asheri kama waliohesabiwa kwao, hamsini na tatu elfu na mia nne. 48 Na wana wa Naftali kwa jamaa zake; wa Yaseeli, jamaa ya Wayaseeli; na wa Guni, jamaa ya Waguni; 49 wa Yeseri, jamaa ya Wayeseri, wa Shilemu jamaa ya Washilemu. 50 Hizi ndizo jamaa za Naftali kwa jamaa zao; na waliohesabiwa kwao walikuwa arobaini na tano elfu na mia nne. 51 Hao ndio waliohesabiwa katika wana wa Israeli, mia sita na moja elfu, na mia saba na thelathini (601,730). 52 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 53 Watu hawa watagawanyiwa nchi hiyo iwe urithi wao, vile vile kama hesabu ya majina yao ilivyo. 54 Hao waliozidi hesabu yao utawapa urithi zaidi, na hao waliopunguka hesabu yao, utawapa urithi kama upungufu wao; kila mtu kama watu wake walivyohesabiwa, ndivyo atakavyopewa urithi wake. 55 Lakini nchi itagawanywa kwa kura; kwa majina ya kabila za baba zao, ndivyo watakavyopata urithi. 56 Kama kura itakavyokuwa, ndivyo urithi wao utakavyogawanywa kati yao, hao wengi na hao wachache. 57 Na hao waliohesabiwa katika Walawi kwa jamaa zao ni hawa; wa Gershoni, jamaa ya Wagershoni; na wa Kohathi, jamaa ya Wakohathi; na wa Merari, jamaa ya Wamerari. 58 Hizi ndizo jamaa za Lawi; jamaa ya Walibni, na jamaa ya Wahebroni, na jamaa ya Wamala, na jamaa ya Wamushi jamaa ya Wakora. Na Kohathi alimzaa Amramu. 59 Na jina la mke wa Amramu aliitwa Yokebedi, binti wa Lawi, ambaye alizaliwa kwake Lawi huko Misri; na huyo Yokebedi akamzalia Amramu Haruni, na Musa, na Miriamu umbu lao. 60 Tena kwake Haruni walizaliwa hawa, Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari. 61 Tena Nadabu na Abihu wakafa, hapo waliposongeza moto wa kigeni mbele za Bwana. 62 Na hao waliohesabiwa kwao walikuwa ishirini na tatu elfu, kila mwanamume tangu huyo aliyepata umri wa mwezi mmoja, na zaidi; kwa kuwa hawakuhesabiwa katika wana wa Israeli, kwa sababu hawakupewa urithi katika wana wa Israeli. 63 Hao ndio waliohesabiwa na Musa na Eleazari kuhani; ambao waliwahesabu wana wa Israeli katika nchi tambarare za Moabu, karibu na Yordani, hapo Yeriko. 64 Lakini katika watu hao hapakuwa na mtu hata mmoja wa wale waliohesabiwa na Musa na Haruni kuhani; waliowahesabu wana wa Israeli katika bara ya Sinai. 65 Kwa kuwa Bwana alisema juu yao, Hapana budi watakufa nyikani. Napo hapakusalia mtu mmoja miongoni mwao, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.

Hesabu 27

1 Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. 2 Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, 3 Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. 4 Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu. 5 Basi Musa akaleta neno lao mbele ya Bwana 6 Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 7 Hao binti za Selofehadi wananena lililo haki; kweli utawapa milki ya urithi pamoja na ndugu za baba yao; nawe utawapa urithi wa baba yao. 8 Kisha utanena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Mtu akifa, naye hana mwana wa kiume, ndipo utampa binti yake urithi wake. 9 Tena ikiwa hana binti, mtawapa nduguze urithi wake. 10 Na ikiwa hana ndugu, mtawapa ndugu za babaye huo urithi wake. 11 Tena ikiwa babaye hana ndugu, utampa huyo aliye karibu naye katika jamaa zake huo urithi wake, naye atakuwa nao; na neno hili litakuwa ni amri ya hukumu kwa wana wa Israeli, kama Bwana alivyomwagiza Musa. 12 Bwana akamwambia Musa, Panda wewe juu ya mlima huu wa Abarimu, uitazame nchi niliyowapa wana wa Israeli. 13 Na ukiisha kuiona, wewe nawe utakusanyika pamoja na baba zako, kama Haruni ndugu yako alivyokusanyika; 14 kwa sababu mliasi juu ya neno langu katika jangwa la Sini wakati wa mateto ya mkutano, wala hamkunistahi, hapo majini, mbele ya macho yao. (Maji hayo ndiyo maji ya Meriba ya Kadeshi katika jangwa la Sini.) 15 Musa akanena na Bwana akisema, 16 Bwana, Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu juu ya mkutano, 17 atakayetoka mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza watokapo, na kuwaleta ndani; ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji. 18 Bwana akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake, ukamwekee mkono wako; 19 kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. 20 Nawe utaweka juu yake sehemu ya heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii. 21 Naye atasimama mbele ya Eleazari kuhani, naye atamwulizia kwa hukumu ya ile Urimu mbele za Bwana; kwa neno lake watatoka, na kwa neno lake wataingia; yeye na wana wa Israeli wote pamoja naye, mkutano wote pia. 22 Musa akafanya kama Bwana alivyomwamuru; akamtwaa Yoshua, akamweka mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; 23 kisha akaweka mikono yake juu yake, akampa mausia, kama Bwana alivyosema kwa mkono wa Musa.

Hesabu 28

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Waagize hao wana wa Israeli, uwaambie, Matoleo yangu, chakula changu cha sadaka zangu zisongezwazo kwa moto, za harufu ya kupendeza kwangu mimi, mtaangalia kuzisongeza kwangu wakati wake upasao. 3 Nawe utawaambia, Hii ndiyo sadaka isongezwayo kwa moto mtakayomsongezea Bwana; wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu, wawili kila siku, wawe sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote. 4 Mwana-kondoo mmoja utamsongeza asubuhi, na mwana-kondoo wa pili utamsongeza jioni; 5 pamoja na sehemu ya kumi ya efa ya unga mwembamba kuwa sadaka ya unga, uliochanganywa na robo ya hini ya mafuta ya kupondwa. 6 Ni sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, iliyoamriwa huko katika mlima wa Sinai iwe harufu ya kupendeza, sadaka ya kusongezwa kwa Bwana kwa moto. 7 Na sadaka yake ya kinywaji itakuwa robo ya hini kwa mwana-kondoo mmoja; hiyo sadaka ya kinywaji, ya kileo, utammiminia Bwana katika mahali hapo patakatifu. 8 Na mwana-kondoo wa pili utamsongeza wakati wa jioni; kama ile sadaka ya unga iliyosongezwa asubuhi, na kama sadaka yake ya kinywaji, ndivyo utakavyoisongeza, ni sadaka ya kusongezwa kwa moto, ni harufu ya kupendeza kwa Bwana. 9 Tena katika siku ya Sabato watasongezwa wana-kondoo wawili, waume wa mwaka wa kwanza, wakamilifu, pamoja na sehemu ya kumi mbili za efa za unga mwembamba kuwa sadaka ya unga, uliochanganywa na mafuta, pamoja na sadaka yake ya kinywaji; 10 hii ndiyo sadaka ya kuteketezwa ya kila Sabato, zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, pamoja na sadaka yake ya kinywaji. 11 Tena katika mianzo ya miezi yenu mtamsongezea Bwana sadaka ya kuteketezwa; nayo ni ng'ombe waume wadogo wawili, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza, wakamilifu, saba; 12 pamoja na sehemu ya kumi tatu za efa za unga mwembamba kuwa sadaka ya unga, uliochanganywa na mafuta, kwa kila ng'ombe; na sehemu ya kumi mbili za unga mwembamba kuwa sadaka ya unga, uliochanganywa na mafuta, kwa huyo kondoo mume mmoja; 13 na sehemu ya kumi moja ya unga mwembamba uliochanganywa na mafuta kuwa sadaka ya unga kwa kila mwana-kondoo; kuwa sadaka ya kuteketezwa ya harufu ya kupendeza, ni sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa njia ya moto. 14 Tena sadaka zake za vinywaji zitakuwa nusu ya hini ya divai kwa ng'ombe, na sehemu ya tatu ya hini kwa kondoo mume, na robo ya hini kwa mwana-kondoo; hii ndiyo sadaka ya kuteketezwa ya kila mwezi katika miezi yote ya mwaka. 15 Tena mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi kwa Bwana itasongezwa zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, pamoja na sadaka yake ya kinywaji. 16 Tena, mwezi wa kwanza, siku ya kumi na nne ya mwezi, ni pasaka ya Bwana. 17 Siku ya kumi na tano ya mwezi huo patakuwa na sikukuu; mkate usiotiwa chachu utaliwa muda wa siku saba. 18 Siku ya kwanza patakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi; 19 lakini mtaisongeza sadaka kwa njia ya moto, sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana; ng'ombe waume wadogo wawili, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza saba; watakuwa wakamilifu kwenu; 20 pamoja na sadaka zake za unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta; mtasongeza sehemu ya kumi tatu kwa ng'ombe mmoja, na sehemu ya kumi mbili kwa kondoo mume; 21 na sehemu ya kumi moja utasongeza kwa kila mwana-kondoo, wale wana-kondoo saba; 22 tena mtasongeza mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi, ili kufanya upatanisho kwa ajili yenu. 23 Mtasongeza wanyama hao zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya asubuhi, iliyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote. 24 Mtasongeza sadaka kwa mfano huu kila siku muda wa siku saba, chakula cha sadaka iliyosongezwa kwa moto, ya harufu ya kupendeza kwa Bwana; itasongezwa zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, pamoja na sadaka yake ya kinywaji. 25 Na siku ya saba mtakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi. 26 Tena katika siku ya malimbuko, hapo mtakapomsongezea Bwana sadaka ya unga mpya katika sikukuu yenu ya majuma mtakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi; 27 lakini mtasongeza sadaka ya kuteketezwa kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe waume wadogo wawili, kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza saba; 28 pamoja na sadaka zake za unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa kila ng'ombe, na sehemu ya kumi mbili kwa kondoo mume, 29 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo, wa wale wana-kondoo saba; 30 na mbuzi mume mmoja, ili kufanya upatanisho kwa ajili yenu. 31 Zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, mtasongeza wanyama hao (watakuwa wakamilifu kwenu), pamoja na sadaka zake za vinywaji.

Hesabu 29

1 Tena mwezi wa saba, siku ya kwanza ya mwezi, mtakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi; ni siku ya kupiga tarumbeta kwenu. 2 Nanyi mtasongeza sadaka ya kuteketezwa kuwa harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe mume mdogo mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu saba; 3 pamoja na sadaka yake ya unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa ng'ombe, sehemu ya kumi mbili kwa kondoo mume, 4 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo katika wale wana-kondoo saba; 5 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi, ili kufanya upatanisho kwa ajili yenu; 6 zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya kuandama mwezi, na sadaka yake ya unga, na hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kama ilivyo amri yake, kuwa harufu ya kupendeza, ni sadaka iliyosongezwa kwa Bwana kwa moto. 7 Tena siku ya kumi ya huo mwezi wa saba mtakuwa na kusanyiko takatifu; nanyi mtazitesa nafsi zenu, msifanye kazi yo yote ya utumishi 8 lakini mtamsongezea Bwana sadaka ya kuteketezwa, kuwa harufu ya kupendeza; ng'ombe mume mdogo mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza saba; watakuwa wakamilifu kwenu; 9 pamoja na sadaka zake za unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa huyo ng'ombe, na sehemu ya kumi mbili kwa huyo kondoo, 10 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo katika wale wana-kondoo saba; 11 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya dhambi ya upatanisho, na hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji. 12 Tena siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba mtakuwa na kusanyiko takatifu; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi, nanyi mtamfanyia Bwana sikukuu muda wa siku saba; 13 nanyi mtasongeza sadaka ya kuteketezwa, sadaka isongezwayo kwa moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe waume wadogo kumi na watatu, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza kumi na wanne; wote watakuwa wakamilifu; 14 pamoja na sadaka zake za unga, unga mwembamba uliochanganywa na mafuta, sehemu ya kumi tatu kwa kila ng'ombe katika wale kumi na watatu na sehemu ya kumi mbili kwa kila kondoo katika hao kondoo waume wawili; 15 na sehemu ya kumi moja kwa kila mwana-kondoo katika wale wana-kondoo kumi na wanne; 16 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji. 17 Tena siku ya pili mtasongeza ng'ombe waume wadogo kumi na wawili, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza kumi na wanne wakamilifu; 18 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuandama hiyo amri; 19 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji. 20 Tena siku ya tatu mtasongeza ng'ombe waume kumi na mmoja, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne; 21 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri; 22 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji. 23 Tena siku ya nne mtasongeza ng'ombe waume kumi, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne; 24 na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri; 25 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi, zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya sikuzote, na sadaka yake ya unga, na sadaka yake ya kinywaji. 26 Tena siku ya tano mtasongeza ng'ombe waume kenda, na kondoo Waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne; 27 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri; 28 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji. 29 Tena siku ya sita mtasongeza ng'ombe waume wanane, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne; 30 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri; 31 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji. 32 Tena siku ya saba mtasongeza ng'ombe waume saba, na kondoo waume wawili, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu kumi na wanne; 33 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa hao ng'ombe, na kwa hao kondoo, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri; 34 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji. 35 Tena siku ya nane mtakuwa na kusanyiko la makini sana; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi; 36 lakini mtasongeza sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya kusongezwa kwa moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng'ombe mume mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu saba; 37 pamoja na sadaka yake ya unga, na sadaka zake za vinywaji, kwa huyo ng'ombe, na kwa huyo kondoo mume, na kwa wale wana-kondoo, kama hesabu yao ilivyo, kwa kuiandama amri; 38 na mbuzi mume mmoja kuwa sadaka ya dhambi; zaidi ya hiyo sadaka ya kuteketezwa ya siku zote, na hiyo sadaka yake ya unga na sadaka yake ya kinywaji. 39 Sadaka hizo mtamsongezea Bwana katika sikukuu zenu zilizoamriwa, zaidi ya nadhiri zenu, na sadaka zenu za hiari, kuwa sadaka zenu za kuteketezwa, na sadaka zenu za unga, na sadaka zenu za vinywaji, na sadaka zenu za amani. 40 Naye Musa akawaambia wana wa Israeli vile vile kama hayo yote Bwana alivyomwagiza Musa.

Hesabu 30

1 Kisha Musa akanena na wale vichwa vya kabila za wana wa Israeli, na kuwaambia, Neno hili ndilo aliloliagiza Bwana. 2 Mtu atakapomwekea Bwana nadhiri, au, atakapoapa kiapo ili kufunga nafsi yake kwa kifungo, asilitangue neno lake; atafanya sawasawa na hayo yote yamtokayo kinywani mwake. 3 Tena mtu mke atakapomwekea Bwana nadhiri, na kufunga nafsi yake kwa kifungo, naye aketi katika nyumba ya babaye, katika ujana wake; 4 babaye naye akasikia nadhiri yake, na kile kifungo chake alichofungia nafsi yake, na babaye akamnyamazia; ndipo nadhiri zake zote zitathibitika, na kila kifungo alichofungia nafsi yake kitathibitika. 5 Lakini kama huyo babaye akimkataza siku hiyo aliyosikia; nadhiri zake ziwazo zote, wala vifungo vyake alivyoifungia nafsi yake havitathibitika; na Bwana atamsamehe, kwa kuwa babaye alimkataza. 6 Tena kama amekwisha kuolewa na mume, wakati huo wa nadhiri zake, au wa neno hilo alilolitamka kwa midomo yake pasipo kufikiri, alilojifungia; 7 na mumewe akasikia, naye akamnyamazia siku hiyo aliyosikia neno hilo; ndipo nadhiri zake zitathibitika, na vile vifungo ambavyo ameifunga nafsi yake vitathibitika. 8 Lakini kama mumewe akimkataza siku hiyo aliyolisikia; ndipo ataitangua nadhiri yake iliyo juu yake na neno alilolitamka kwa midomo yake pasipo kufikiri, alilojifungia; na Bwana atamsamehe 9 Lakini nadhiri ya mjane, au ya mwanamke aliyeachishwa mume, kila neno ambalo ameifunga nafsi yake kwalo, litathibitika juu yake. 10 Tena kama aliweka nadhiri nyumbani mwa mumewe, au kama aliifunga nafsi yake kwa kifungo pamoja na kiapo, 11 na mumewe alisikia akamnyamazia, wala hakumkataza; ndipo nadhiri zake zote zitathibitika, na kila kifungo alichojifungia kitathibitika. 12 Lakini kama mumewe alizibatilisha na kuzitangua siku hiyo aliyozisikia, ndipo kila neno lililotoka midomoni mwake katika hizo nadhiri zake, au katika kile kifungo cha nafsi yake, halitathibitika; huyo mumewe amezitangua; na Bwana atamsamehe. 13 Kila nadhiri, na kila kiapo kifungacho, ili kuitaabisha nafsi ya mwanamke mumewe aweza kuthibitisha, au mumewe aweza kutangua. 14 Lakini mumewe akimnyamazia mkewe kabisa siku hata siku ndipo azithibitisha nadhiri zote za mkewe, au vifungo vyake vyote vilivyo juu yake; yeye amezithibitisha, kwa kuwa alimnyamazia mkewe siku hiyo aliyozisikia nadhiri zake. 15 Lakini akizibatilisha na kuzitangua baada ya kuzisikia; ndipo yeye atachukua uovu wa mkewe. 16 Hizi ndizo amri, ambazo Bwana alimwagiza Musa, kati ya mtu mume na mkewe, kati ya baba na binti yake, katika ujana wake, ali nyumbani mwa babaye.

Hesabu 31

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Walipize kisasi wana wa Israeli juu ya Wamidiani; kisha baadaye utakusanywa uwe pamoja na watu wako. 3 Basi Musa akanena na watu, na kuwaambia, Wavikeni silaha watu miongoni mwenu waende vitani, ili waende kupigana na Midiani, wapate kumlipiza kisasi Bwana, juu ya Midiani. 4 Katika kila kabila mtatoa watu elfu, katika kabila zote za Israeli, nanyi mtawapeleka waende vitani. 5 Basi walitolewa katika maelfu ya Israeli, elfu moja ya kila kabila, watu waume kumi na mbili elfu walioandaliwa kwa vita. 6 Basi Musa akawapeleka, watu elfu wa kila kabila waende vitani, wao na Finehasi mwana wa Eleazari kuhani, waende vitani, na vile vyombo vya mahali patakatifu, na hizo tarumbeta za kupiga sauti za kugutusha mkononi mwake. 7 Nao wakapigana na Midiani kama Bwana alivyomwagiza Musa; nao wakamwua kila mume. 8 Nao wafalme wa Midiani wakawaua pamoja na watu wengine waliouawa; Evi, na Rekemu, na Suri, na Huri, na Reba, hao wafalme watano wa Midiani; Balaamu mwana wa Beori naye wakamwua kwa upanga. 9 Wana wa Israeli wakawachukua mateka wanawake wa Midiani na watoto wao; na ng'ombe zao wote, na kondoo zao wote, na mali zao zote, wakachukua nyara. 10 Na miji yao yote, kila mahali walipokuwa wakikaa, na marago yao yote wakayateketeza kwa moto. 11 Nao wakatwaa hizo nyara zote, na mateka yote, ya wanadamu na ya wanyama. 12 Nao wakawaleta mateka ya wanadamu, na mateka ya wanyama, na hizo nyara, na kuyaweka mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wa wana wa Israeli, hapo maragoni katika nchi tambarare za Moabu, zilizo karibu na Yordani hapo Yeriko. 13 Basi Musa, na Eleazari kuhani, na wakuu wote wa huo mkutano, wakatoka nje kwenda kuwalaki nje ya marago. 14 Musa akawakasirikia majemadari wa jeshi, na hao maakida wa elfu elfu, na wakuu wa mia mia, hao waliorudi kutoka katika kupiga vita. 15 Musa akawauliza, Je! Mmewaponya wanawake wote hai? 16 Tazama, hawa ndio waliowakosesha wana wa Israeli, kwa shauri la Balaamu, wamfanyie Bwana dhambi katika hilo jambo la Peori, na kwa hivyo pigo lilikuwa katika mkutano wa Bwana. 17 Basi kwa ajili hiyo mwueni kila mume katika hao watoto, na kila mwanamke aliyemjua mume kwa kulala pamoja naye. 18 Lakini hao watoto wote wa kike ambao hawakumjua mume kwa kulala pamoja naye, mtawaweka hai kwa ajili yenu. 19 Nanyi fanyeni matuo yenu nje ya marago muda wa siku saba; mtu awaye yote aliyemwua mtu, na awaye yote aliyemgusa mtu aliyeuawa, jitakaseni nafsi zenu siku ya tatu, na siku ya saba, ninyi na mateka yenu. 20 Na katika habari ya kila nguo, na kila kitu kilichofanywa cha ngozi, na kazi yote ya singa za mbuzi, na vyombo vyote vilivyofanywa vya mti, mtajitakasa wenyewe; 21 Kisha Eleazari kuhani akawaambia waume wa vita wote waliokwenda vitani, Hii ndiyo amri ya sheria Bwana aliyomwagiza Musa; 22 lakini dhahabu, na fedha, na shaba, na chuma, na bati, na risasi, 23 kila kitu kiwezacho kuuhimili moto, mtakipitisha katika moto, nacho kitakuwa safi, pamoja na haya kitatakaswa kwa hayo maji ya farakano; na kila kitu kisichouhimili moto mtakipitisha katika hayo maji. 24 Nanyi mtazifua nguo zenu siku ya saba, nanyi mtakuwa safi, kisha baadaye mtaingia maragoni. 25 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 26 Fanya jumla ya hayo mateka ya wanadamu, na ya wanyama pia, wewe, na Eleazari kuhani, na wakuu wa nyumba za baba za mkutano; 27 ukagawanye nyara mafungu mawili; kati ya watu waliozoea vita, waliotoka nje waende vitani, na huo mkutano wote; 28 kisha uwatoze hao watu wa vita waliotoka kwenda vitani sehemu kwa ajili ya Bwana; mmoja katika mia tano, katika wanadamu, na katika ng'ombe, na katika punda, na katika kondoo; 29 twaa katika nusu yao, ukampe Eleazari kuhani, kuwa sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana. 30 Na katika hiyo nusu ya wana wa Israeli utatwaa mmoja atakayetolewa katika kila hamsini, katika wanadamu, na katika ng'ombe, na katika punda, na katika kondoo, maana, katika wanyama wote, ukawape Walawi, hao walindao ulinzi wa maskani ya Bwana. 31 Musa na Eleazari kuhani wakafanya kama Bwana alivyomwagiza Musa. 32 Basi masazo ya hizo nyara walizotwaa watu wa vita, zilikuwa ni kondoo mia sita na sabini na tano elfu, 33 na ng'ombe sabini na mbili elfu, 34 na punda sitini na moja elfu, 35 tena wanadamu jumla yao ilikuwa thelathini na mbili elfu, katika hao wanawake ambao hawakumjua mume kwa kulala pamoja naye. 36 Na hiyo nusu ambayo ilikuwa ni sehemu ya hao waliotoka kwenda vitani, hesabu yake ilikuwa kondoo mia tatu na thelathini na saba elfu na mia tano; 37 na kodi ya Bwana katika hao kondoo ilikuwa kondoo mia sita na sabini na watano. 38 Tena, ng'ombe walikuwa thelathini na sita elfu; na katika hao kodi ya Bwana ilikuwa ng'ombe sabini na wawili. 39 Na punda walikuwa thelathini elfuna mia tano, katika hao kodi ya Bwana ilikuwa punda sitini na mmoja. 40 Na wanadamu walikuwa watu kumi na sita elfu; katika hao sehemu ya Bwana ilikuwa ni watu thelathini na wawili. 41 Basi Musa akampa Eleazari kuhani hiyo sehemu, iliyokuwa sadaka ya kuinuliwa kwa Bwana, kama Bwana alivyomwagiza Musa. 42 Tena katika hiyo nusu iliyokuwa ya wana wa Israeli, ambayo Musa aliitenga na watu waliokwenda vitani, 43 (basi hiyo nusu ya mkutano ilikuwa ni kondoo mia tatu na thelathini na saba elfu na mia tano, 44 na ng'ombe thelathini na sita elfu, 45 na punda thelathini elfu, na mia tano, 46 na wanadamu kumi na sita elfu;) 47 na katika hiyo nusu iliyokuwa ya wana wa Israeli, Musa akatwaa mmoja aliyetolewa katika kila hamsini, wa binadamu na wa wanyama, akawapa Walawi, waliolinda ulinzi wa maskani ya Bwana; kama Bwana alivyomwagiza Musa. 48 Na majemadari waliokuwa juu ya elfu elfu za hiyo jeshi, na maakida wa elfu elfu, na maakida wa mia mia, wakamkaribia Musa; 49 wakamwambia Musa wakisema, Sisi watumishi wako tumefanya jumla ya hesabu ya watu wa vita walio chini ya mikono yetu, na hapana hata mmoja aliyetupungukia. 50 Nasi tumeleta matoleo ya Bwana, aliyopata kila mtu, ya vyombo vya dhahabu, na mitali, na timbi, na pete za muhuri, na vipini, na vikuku, ili kuzifanyia upatanisho nafsi zetu mbele ya Bwana. 51 Musa na Eleazari kuhani wakapokea kwao hiyo dhahabu, maana, vile vyombo vyote vilivyofanyizwa. 52 Na dhahabu yote ya sadaka ya kuinuliwa waliyosongeza kwa Bwana, ya maakida wa elfu elfu, na maakida wa mia mia, ilikuwa shekeli kumi na sita elfu na mia saba na hamsini. 53 (Kwa kuwa hao watu wa vita walikuwa wametwaa nyara, kila mtu nafsi yake.) 54 Basi Musa na Eleazari kuhani wakapokea hiyo dhahabu mikononi mwa hao maakida wa elfu elfu na wa mia mia, na kuileta ndani ya hema ya kukutania, ili iwe ukumbusho kwa ajili ya wana wa Israeli mbele za Bwana.

Hesabu 32

1 Basi wana wa Reubeni, na hao wana wa Gadi, walikuwa na wanyama wa mifugo wengi sana; nao walipoona nchi ya Yazeri, na nchi ya Gileadi, ya kuwa mahali hapo palikuwa ni mahali pa kuwafaa wanyama; 2 hao wana wa Gadi, na wana wa Reubeni, wakamwendea Musa na Eleazari kuhani, na wakuu wa mkutano, wakanena nao, wakisema, 3 Atarothi, na Diboni, na Yazeri, na Nimra, na Heshboni, na Eleale, na Sebamu, na Nebo na Beoni, 4 nchi hiyo ambayo Bwana aliipiga mbele ya mkutano wa Israeli, ni nchi ifaayo kwa mfugo wa wanyama, nasi watumishi wako tuna wanyama. 5 Wakasema, Kama tumepata kibali mbele ya macho yako, sisi watumishi wako na tupewe nchi hii iwe milki yetu; usituvushe mto wa Yordani. 6 Musa akawaambia wana wa Gadi na wana wa Reubeni, Je! Ndugu zenu waende vitani nanyi mtaketi hapa? 7 Mbona mwawavunja mioyo yao wana wa Israeli, wasivuke na kuingia nchi hiyo ambayo Bwana amewapa? 8 Ndivyo walivyofanya baba zenu, hapo nilipowatuma kutoka Kadesh-barnea ili waende kuiangalia hiyo nchi. 9 Kwa kuwa walipokwea na kuingia bonde la Eshkoli, na kuiona nchi, wakawavunja mioyo wana wa Israeli, ili wasikwee kuingia nchi Bwana aliyowapa. 10 Na siku ile hasira za Bwana ziliwaka, naye akaapa, akisema, 11 Hakika yangu hapana mtu mmoja katika wale watu waliotoka Misri, tangu huyo aliyepata umri wa miaka ishirini, na zaidi, atakayeiona hiyo nchi niliyomwapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo; kwa sababu hawakuniandama kwa moyo wote; 12 ila Kalebu mwana wa Yefune, Mkenizi, na Yoshua mwana wa Nuni; kwa kuwa wao wamemwandama Bwana kwa moyo wote. 13 Na hasira za Bwana ziliwaka juu ya Israeli, naye akawatembeza huku na huku jangwani muda wa miaka arobaini, hata kizazi hicho kizima kilichokuwa kimefanya uovu machoni pa Bwana kikaisha angamia. 14 Na tazama, ninyi mmeinuka badala ya baba zenu, maongeo ya watu wenye dhambi, ili kuongeza tena hizo hasira kali za Bwana juu ya Israeli. 15 Kwa kuwa mkigeuka msimwandame, yeye atawaacha tena nyikani; nanyi mtawaangamiza watu hawa wote. 16 Basi wakamwendea karibu, na kusema, Sisi tutafanya mazizi hapa kwa ajili ya wanyama wetu wa mifugo, na kujenga miji kwa ajili ya watoto wetu; 17 lakini sisi wenyewe tutakuwa tayari na silaha zetu kutangulia mbele ya wana wa Israeli, hata tutakapowafikisha mahali pao; na watoto wetu watakaa katika hiyo miji yenye maboma, kwa sababu ya wenyeji wa nchi. 18 Sisi hatutarudia nyumba zetu, hata wana wa Israeli watakapokuwa wamekwisha kurithi kila mtu urithi wake. 19 Kwa kuwa sisi hatutarithi pamoja nao huko ng'ambo ya pili ya Yordani, huko mbele; kwa sababu urithi wetu umetuangukia upande huu wa Yordani kwa mashariki. 20 Basi Musa akawaambia, Kama mtafanya jambo hili; kama mtajivika silaha, ili kutangulia mbele ya Bwana mwende vitani, 21 tena kama kila mume wa kwenu mwenye kuchukua silaha atavuka Yordani mbele ya Bwana, hata atakapokuwa amekwisha watoa adui zake mbele yake, 22 na hiyo nchi kushindwa mbele za Bwana; ndipo baadaye mtarudi, nanyi mtakuwa hamna hatia mbele za Bwana, wala kwa Israeli; na nchi hii itakuwa milki yenu mbele za Bwana. 23 Lakini kama hamtaki kufanya neno hilo, ninyi mmefanya dhambi mbele za Bwana, nanyi jueni ya kwamba hiyo dhambi yenu itawapata hapana budi. 24 Basi, jengeni miji kwa ajili ya watoto wenu, na mazizi kwa ajili ya kondoo zenu; mkayafanye hayo mliotamka kwa vinywa vyenu. 25 Ndipo wana wa Gadi na wana wa Reubeni wakanena na Musa, na kumwambia, Sisi watumishi wako tutafanya kama wewe bwana wangu utuagizavyo. 26 Watoto wetu, na wake wetu, na kondoo zetu, na ng'ombe zetu wote, watakuwa hapo katika miji ya Gileadi; 27 lakini sisi watumishi wako tutavuka, kila mume aliyevaa silaha za vita, mbele za Bwana, tuende vitani, kama wewe bwana wangu usemavyo. 28 Basi Musa akamwagiza Eleazari kuhani, na Yoshua mwana wa Nuni, na wakuu wa nyumba za mababa za kabila za wana wa Israeli, katika habari za watu hao. 29 Musa akawaambia, Kwamba wana wa Gadi, na wana wa Reubeni, watavuka Yordani pamoja nanyi, kila mtu aliyevaa silaha kwa vita, mbele za Bwana, nayo nchi itashindwa mbele yenu; ndipo mtawapa nchi ya Gileadi kuwa milki yao; 30 lakini ikiwa hawataki kuvuka pamoja nanyi, hali wamevaa silaha zao, ndipo watakuwa na milki zao kati yenu katika nchi ya Kanaani. 31 Wana wa Gadi, na wana wa Reubeni, wakajibu na kusema, Kama Bwana alivyotuambia sisi watumishi wako, ndivyo tutakavyofanya. 32 Tutavuka, hali tumevaa silaha zetu, mbele za Bwana, kuingia nchi ya Kanaani, nayo milki ya urithi wetu itakuwa ng'ambo ya pili ya Yordani. 33 Basi Musa akawapa wao, maana, wana wa Gadi, na wana wa Reubeni, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, mwana wa Yusufu, ufalme wa Sihoni mfalme wa Waamori, na ufalme wa Ogu mfalme wa Bashani, hiyo nchi, kama miji yao ilivyokuwa, pamoja na mipaka yake, maana, miji ya hiyo nchi iliyozunguka kotekote. 34 Kisha wana wa Gadi wakajenga Diboni, na Atarothi, na Aroeri; 35 na Atrothi-shofani, na Yazeri, na Yogbeha; 36 na, Beth-nimra, na Beth-harani; miji yenye maboma, na mazizi ya kondoo. 37 Na wana wa Reubeni wakajenga Heshboni, na Eleale, na Kiriathaimu; 38 na Nebo, na Baal-meoni, (majina yake yalikuwa yamegeuzwa) na Sibma; nao wakaiita miji waliyoijenga majina mengine. 39 Na wana wa Makiri mwana wa Manase wakaenda Gileadi, na kuitwaa, na kuwapokonya Waamori waliokuwamo humo. 40 Basi Musa akampa Makiri, mwana wa Manase, Gileadi, naye akakaa humo. 41 Kisha Yairi mwana wa Manase akaenda na kuvitwaa vijiji vya Gileadi. Akaviita jina lake Hawoth-yairi. 42 Kisha Noba akaenda na kutwaa Kenathi na vijiji vyake, na kuita jina lake Noba, kwa kuandama jina lake mwenyewe.

Hesabu 33

1 Hizi ndizo safari za wana wa Israeli, hapo walipotoka nchi ya Misri kwa jeshi zao chini ya mkono wa Musa na Haruni. 2 Musa akaandika jinsi walivyotoka katika safari zao, kwa amri ya Bwana; na hizi ndizo safari zao kama kutoka kwao kulivyokuwa. 3 Wakasafiri kutoka Ramesesi mwezi wa kwanza, siku ya kumi na tano ya mwezi wa kwanza; siku ya pili baada ya Pasaka, wana wa Israeli wakatoka kwa mkono wa nguvu mbele ya macho ya Wamisri wote, 4 hapo Wamisri walipokuwa wanazika wazaliwa wa kwanza wao wote, Bwana aliokuwa amewapiga kati yao; Bwana akafanya hukumu juu ya miungu yao nayo. 5 Wana wa Israeli wakasafiri kutoka Ramesesi, wakapanga katika Sukothi. 6 Kisha wakasafiri kutoka Sukothi, wakapanga Ethamu, palipo katika mwisho wa nyika. 7 Wakasafiri kutoka Ethamu, na kurudi nyuma hata Pi-hahirothi palipokabili Baal-sefoni; wakapanga mbele ya Migdoli. 8 Wakasafiri kutoka hapo mbele ya Hahirothi, wakapita katikati ya bahari na kuingia jangwani; kisha wakaenda safari ya siku tatu katika nyika ya Ethamu, wakapanga Mara. 9 Wakasafiri kutoka Mara, wakafikilia Elimu; huko Elimu palikuwa na chemchemi za maji kumi na mbili, na mitende sabini; nao wakapanga hapo. 10 Wakasafiri kutoka Elimu wakapanga karibu na Bahari ya Shamu. 11 Wakasafiri kutoka Bahari ya Shamu, wakapanga katika nyika ya Sini. 12 Wakasafiri kutoka nyika ya Sini, wakapanga Dofka. 13 Wakasafiri kutoka Dofka, wakapanga Alushi. 14 Wakasafiri kutoka Alushi, wakapanga Refidimu, ambapo hapakuwa na maji ya watu kunywa. 15 Wakasafiri kutoka Refidimu, wakapanga katika nyika ya Sinai. 16 Wakasafiri kutoka nyika ya Sinai, wakapanga Kibroth-hataava. 17 Wakasafiri kutoka Kibroth-hataava, wakapanga Haserothi. 18 Wakasafiri kutoka Haserothi, wakapanga Rithma. 19 Wakasafiri kutoka Rithma, wakapanga Rimon-peresi. 20 Wakasafiri kutoka Rimon-peresi, wakapanga Libna. 21 Wakasafiri kutoka Libna, wakapanga Risa. 22 Wakasafiri kutoka Risa, wakapanga Keheletha. 23 Wakasafiri kutoka Keheletha, wakapanga katika mlima wa Sheferi 24 Wakasafiri kutoka huo mlima wa Sheferi, wakapanga Harada. 25 Wakasafiri kutoka Harada, wakapanga Makelothi. 26 Wakasafiri kutoka Makelothi, wakapanga Tahathi. 27 Wakasafiri kutoka Tahathi wakapanga Tera. 28 Wakasafiri kutoka Tera, wakapanga Mithka. 29 Wakasafiri kutoka Mithka, wakapanga Hashmona. 30 Wakasafiri kutoka Hashmona, wakapanga Moserothi. 31 Wakasafiri kutoka Moserothi, wakapanga Bene-yakani. 32 Wakasafiri kutoka Bene-yakani, wakapanga Hor-hagidgadi. 33 Wakasafiri kutoka Hor-hagidgadi, wakapanga Yotbatha. 34 Wakasafiri kutoka Yotbatha, wakapanga Abrona. 35 Wakasafiri kutoka Abrona, wakapanga Esion-geberi. 36 Wakasafiri kutoka Esion-geberi, wakapanga katika nyika ya Sini (ni Kadeshi). 37 Wakasafiri kutoka Kadeshi wakapanga katika mlima wa Hori, katika mpaka wa nchi ya Edomu, 38 Haruni akakwea mlima wa Hori, kwa amri ya Bwana, akafa hapo, katika mwaka wa arobaini baada ya wana wa Israeli kutoka katika nchi ya Misri, mwezi wa tano, siku ya kwanza ya mwezi. 39 Naye Haruni alikuwa mtu wa umri wa miaka mia na ishirini na mitatu hapo alipokufa katika mlima wa Hori. 40 Ndipo Mkanaani, mfalme wa Aradi, aliyekaa pande za Negebu katika nchi ya Kanaani akasikia habari za kuja kwao wana wa Israeli. 41 Nao wakasafiri kutoka mlima wa Hori, wakapanga Salmona. 42 Wakasafiri kutoka Salmona, wakapanga Punoni. 43 Wakasafiri kutoka Punoni, wakapanga Obothi. 44 Wakasafiri kutoka Obothi, wakapanga Iye-abarimu, katika mpaka wa Moabu. 45 Wakasafiri kutoka Iye-abarimu, wakapanga Dibon-gadi. 46 Wakasafiri kutoka Dibon-gadi, wakapanga Almon-diblathaimu. 47 Wakasafiri kutoka Almon-diblathaimu, wakapanga katika milima ya Abarimu, kukabili Nebo. 48 Wakasafiri kutoka hiyo milima ya Abarimu, wakapanga katika nchi tambarare za Moabu, karibu na mto wa Yordani, hapo Yeriko. 49 Wakapanga karibu na Yordani, tangu Beth-yeshimothi hata kufikilia Abel-shitimu katika nchi tambarare za Moabu. 50 Kisha Bwana akanena na Musa hapo katika nchi tambarare za Moabu, karibu na Yordani, hapo Yeriko, na kumwambia, 51 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapovuka mto wa Yordani na kuingia nchi ya Kanaani, 52 ndipo mtakapowafukuza wenyeji wote wa hiyo nchi mbele yenu, nanyi mtayaharibu mawe yao yote yenye kuchorwa sanamu, na kuziharibu sanamu zao zote za kusubu, kuvunja-vunja mahali pao pote palipoinuka; 53 nanyi mtaishika hiyo nchi kuimiliki na kuketi humo; kwa kuwa mimi nimewapa ninyi hiyo nchi ili mwimiliki. 54 Nanyi mtairithi nchi kwa kufanya kura, kama jamaa zenu zilivyo; hao walio wengi mtawapa urithi zaidi, na hao waliopunguka utawapa kama kupunguka kwao; mahali po pote kura itakapomwangukia mtu ye yote, mahali hapo ni pake; mtarithi kama kabila za baba zenu zilivyo. 55 Lakini kama hamtaki kuwafukuza wenyeji wa nchi watoke mbele yenu; ndipo hao ambao mtakaowasaza watakuwa kama sindano machoni mwenu, na kama miiba ubavuni mwenu, nao watawasumbua katika hiyo nchi ambayo mwakaa. 56 Kisha itakuwa, kama nilivyoazimia kuwatenda wao, ndivyo nitakavyowatenda ninyi.

Hesabu 34

1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 2 Waagize wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapoingia nchi ya Kanaani, (hii ndiyo nchi itakayowaangukia kuwa urithi, maana, hiyo nchi ya Kanaani kama mipaka yake ilivyo,) 3 ndipo upande wenu wa kusini utakuwa tangu bara ya Sini kupita kando ya Edomu, na mpaka wenu wa kusini utakuwa tangu mwisho wa Bahari ya Chumvi kuelekea mashariki; 4 kisha mpaka wenu utageuka kwenda upande wa kusini wa kukwelea kwake Akrabimu, kisha kupita kwendelea Sini; na kutokea kwake kutakuwa kuelekea upande wa kusini wa Kadesh-barnea; kisha utaendelea mpaka Hasar-adari, na kufikilia Azmoni; 5 kisha mpaka utageuka kutoka Azmoni kwendelea kijito cha Misri, na kutokea kwake kutakuwa hapo baharini. 6 Kisha mpaka wenu wa upande wa magharibi mtakuwa na bahari kubwa na mpaka wake; hii ndiyo mpaka wenu upande wa magharibi. 7 Kisha mpaka wenu wa upande wa kaskazini utakuwa ni huu; kutoka bahari kubwa mtajiandikia mlima wa Hori; 8 na kutoka mlima wa Hori mtaandika mpaka kuingilia kwake Hamathi; na kutokea kwake mpaka kutakuwa hapo Sedada; 9 tena mpaka utatokea hata Zifroni, na kutokea kwake kutakuwa hapo Hasarenani; huo ndio mpaka wenu wa upande wa kaskazini. 10 Kisha mtaandika mpaka wenu wa upande wa mashariki kutoka Hasarenani hata Shefamu; 11 kisha mpaka utatelemka kutoka Shefamu mpaka Ribla, upande wa mashariki wa Aini; kisha mpaka utatelemka na kufikilia upande wa bahari ya Kinerethi upande wa mashariki; 12 kisha mpaka utatelemkia Yordani, na kutokea kwake kutakuwa hapo katika Bahari ya Chumvi; hii ndiyo nchi yenu kama mipaka yake ilivyo kuizunguka pande zote. 13 Kisha Musa akawaagiza wana wa Israeli, akisema, Hii ndiyo nchi mtakayoirithi kwa kupiga kura, ambayo Bwana ameagiza wapewe watu wa zile kabila kenda, na nusu ya kabila; 14 kwa kuwa kabila ya wana wa Reubeni kwa nyumba za baba zao, na kabila ya wana wa Gadi kwa nyumba za baba zao, wamekwisha pata, na hiyo nusu ya kabila ya Manase wamekwisha pata urithi wao; 15 hizo kabila mbili na nusu ya kabila wamekwisha pata urithi wao huko ng'ambo ya pili ya Yordani, hapo Yeriko, upande wa mashariki, kuelekea maawio ya jua. 16 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 17 Haya ndiyo majina ya watu watakaowagawanyia nchi iwe urithi wenu; Eleazari kuhani, na Yoshua mwana wa Nuni. 18 Kisha mtamtwaa mkuu mmoja wa kila kabila, ili waigawanye nchi iwe urithi wenu. 19 Na majina ya watu hao ni haya; katika kabila ya Yuda, ni Kalebu mwana wa Yefune. 20 Na katika kabila ya wana wa Simeoni, Shemueli mwana wa Amihudi. 21 Katika kabila ya Benyamini, ni Elidadi mwana wa Kisloni. 22 Na katika kabila ya wana wa Dani, mkuu, Buki mwana wa Yogli. 23 Katika wana wa Yusufu; katika kabila ya wana wa Manase, mkuu, Hanieli mwana wa Efodi; 24 na katika kabila ya wana wa Efraimu, mkuu, Kemueli mwana wa Shiftani. 25 Na katika kabila ya wana wa Zabuloni, mkuu, Elisafani mwana wa Parnaki. 26 Na katika kabila ya wana wa Isakari, mkuu, Paltieli mwana wa Azani. 27 Na katika kabila ya wana wa Asheri, mkuu, Ahihudi mwana wa Shelomi. 28 Na katika kabila ya wana wa Naftali, mkuu, Pedaheli mwana wa Amihudi. 29 Hao ndio Bwana aliowaagiza wawagawanyie urithi wana wa Israeli katika nchi ya Kanaani.

Hesabu 35

1 Kisha Bwana akanena na Musa katika nchi tambarare za Moabu, karibu na mto wa Yordani, hapo Yeriko, akamwambia, 2 Uwaagize wana wa Israeli wawape Walawi miji wapate mahali pa kukaa, katika milki yao; pamoja na malisho yaliyoizunguka hiyo miji kotekote mtawapa Walawi. 3 Hiyo miji watakuwa nayo ili wakae humo, na malisho watakuwa nayo kwa wanyama wao wa mifugo, na kwa mali zao, na kwa wanyama wao wote. 4 Na yale malisho ya miji mtakayowapa Walawi, ukubwa wake utakuwa tangu ukuta wa mji kupima kiasi cha dhiraa elfu pande zote. 5 Nanyi mtapima hapo nje ya mji upande wa mashariki dhiraa elfu mbili, na upande wa kusini dhiraa elfu mbili, na upande wa magharibi dhiraa elfu mbili, na upande wa kaskazini dhiraa elfu mbili, huo mji ulio katikati. Hayo ndiyo yatakayokuwa kwao malisho ya miji. 6 Na hiyo miji mtakayowapa Walawi, itakuwa miji sita ya makimbilio, mtakayoweka kwa ajili ya mwenye kumwua mtu, ili akimbilie huko; pamoja na hiyo mtawapa miji arobaini na miwili zaidi. 7 Miji yote mtakayowapa hao Walawi jumla yake itakuwa miji arobaini na minane; mtawapa miji hiyo pamoja na malisho yake. 8 Tena katika miji mtakayotoa ya hiyo milki ya wana wa Israeli, katika hao walio wengi mtatwaa miji mingi; na katika hao walio wachache mtatwaa miji michache; kila mtu kama ulivyo urithi wake atakaourithi, atawapa Walawi katika miji yake. 9 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, 10 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapovuka mto wa Yordani na kuingia nchi ya Kanaani, 11 Ndipo mtajiwekea miji iwe miji ya makimbilio kwa ajili yenu; ili kwamba mwenye kumwua mtu, pasipo kukusudia kumwua, apate kukimbilia huko. 12 Na hiyo miji itakuwa kwenu kuwa makimbilio, kumkimbia mwenye kutwaa kisasi, ili asiuawe mwenye kumwua mtu, hata atakaposimama mbele ya mkutano ahukumiwe. 13 Na hiyo miji mtakayowapa itakuwa kwenu ni miji sita ya makimbilio. 14 Mtawapa miji mitatu ng'ambo ya pili ya Yordani, na miji mitatu mtawapa katika nchi ya Kanaani; miji hiyo itakuwa ni miji ya makimbilio. 15 Miji hiyo sita itakuwa miji ya makimbilio kwa ajili ya wana wa Israeli, na kwa ajili ya mgeni, na kwa ajili ya huyo aketiye kati yao hali ya ugeni; ili kila amwuaye mtu, naye hakukusudia kumwua, apate kukimbilia huko. 16 Lakini kama alimpiga kwa chombo cha chuma, akafa, ni mwuaji huyo; mwuaji hakika yake atauawa. 17 Na kama alimpiga kwa jiwe lililokuwa mkononi mwake, ambalo kwa hilo humkini mtu kufa, naye akafa, yeye ni mwuaji; huyo mwuaji lazima atauawa. 18 Au kama alimpiga kwa chombo cha mti kilichokuwa mkononi mwake ambacho kwa hicho humkini mtu kufa, naye akafa, ni mwuaji huyo, mwuaji lazima atauawa. 19 Mwenye kutwaa kisasi cha damu ndiye atakayemwua mwuaji; hapo atakapokutana naye, atamwua. 20 Tena kwamba alimsukuma kwa kumchukia, au kwamba alimtupia kitu kwa kumvizia, hata akafa; 21 au akampiga kwa mkono wake kwa kuwa ni adui, naye akafa; yeye aliyempiga lazima atauawa; yeye ni mwuaji; mwenye kutwaa kisasi cha damu atamwua mwuaji, hapo atakapokutana naye. 22 Lakini ikiwa alimsukuma ghafula pasipo kumchukia; au akamtupia kitu cho chote pasipo kumvizia, 23 au kwa jiwe liwalo lote, ambalo kwa kupigwa kwalo humkini mtu kufa, asipomwona, akamtupia hata akafa, naye hakuwa adui yake, wala hakumtakia madhara; 24 ndipo mkutano utaamua kati ya huyo aliyempiga mtu na huyo atakayetwaa kisasi cha damu, kama hukumu hizi zilivyo; 25 nao mkutano utamwokoa yule aliyemwua mtu na mkono wa mwenye kutwaa kisasi cha damu; tena mkutano utamrejeza katika mji wake wa makimbilio, aliokuwa anaukimbilia; naye atakaa humo hata kifo chake kuhani mkuu, aliyepakwa mafuta kwa mafuta matakatifu. 26 Lakini kama mwenye kumwua mtu akienda wakati wo wote kupita mpaka wa huo mji wa makimbilio, alioukimbilia; 27 na mwenye kutwaa kisasi cha damu akamwona, naye yu nje ya mpaka wa mji wake wa makimbilio, na mwenye kutwaa kisasi cha damu akamwua huyo mwuaji, hatakuwa na hatia ya damu; 28 kwa sababu ilimpasa kukaa ndani ya mji wake wa makimbilio hata kifo chake kuhani mkuu lakini kuhani mkuu atakapokwisha kufa huyo mwuaji atarudi aende nchi ya urithi wake. 29 Mambo haya yatakuwa ni amri ya hukumu kwenu, katika vizazi vyenu vyote, katika makazi yenu yote. 30 Mtu awaye yote atakayemwua mtu, huyo mwuaji atauawa kwa vinywa vya mashahidi; lakini shahidi mmoja hatashuhudia juu ya mtu hata akafa. 31 Tena, msipokee fidia kwa ajili ya uhai wa mwuaji, ambaye amekuwa na hatia ya mauti; Lakini lazima atauawa. 32 Tena hamtapokea fidia kwa ajili ya huyo aliyeukimbilia mji wake wa makimbilio, apate kwenda tena kuketi katika nchi, hata kifo cha kuhani mkuu. 33 Hivi hamtaitia unajisi nchi ambayo mwakaa; kwa kuwa damu huitia nchi unajisi; wala hapana sadaka itoshayo kwa ajili ya nchi, kwa ajili ya damu iliyomwagwa ndani yake, isipokuwa ni damu ya huyo aliyeimwaga. 34 Kwa hiyo msiitie unajisi nchi muiketiyo, ambayo naketi nami kati yake; kwa kuwa mimi Bwana nakaa kati ya wana wa Israeli.

Hesabu 36

1 Kisha wale wakuu wa nyumba za mababa ya jamaa ya wana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, katika jamaa za wana wa Yusufu, wakakaribia, na kunena mbele ya Musa, na mbele ya wakuu walio juu ya nyumba za mababa ya wana wa Israeli; 2 wakasema, Bwana alimwagiza bwana wangu awape wana wa Israeli nchi kwa kupiga kura iwe urithi wao; tena bwana wangu aliagizwa na Bwana awape binti za Selofehadi ndugu yetu huo urithi wa baba yao. 3 Wakiolewa na watu wa wana wa hizo kabila nyingine za wana wa Israeli, ndipo urithi wao utatwaliwa na kuondolewa katika urithi wa baba zetu, na hiyo kabila watakayotiwa ndani yake itaongezewa urithi wao; basi urithi huo utaondolewa katika kura ya urithi wetu. 4 Tena itakapokuwapo hiyo yubile ya wana wa Israeli, ndipo urithi wa hiyo kabila ambayo wamekuwa ndani yake utaongezewa huo urithi wao; hivyo urithi wao utaondolewa katika urithi wa kabila ya baba zetu. 5 Basi Musa akawaagiza wana wa Israeli kama neno la Bwana lilivyokuwa, akasema, Kabila ya wana wa Yusufu imenena yaliyo haki. 6 Bwana ameagiza neno hili katika habari ya binti za Selofehadi, akasema, Na waolewe na waume wawapendao; lakini na waolewe katika jamaa ya kabila ya baba zao. 7 Hivyo hapana urithi wo wote wa wana wa Israeli utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa wana wa Israeli watashikamana kila mtu na urithi wa kabila ya baba zake. 8 Na kila binti atakayemiliki urithi katika kabila yo yote katika wana wa Israeli, ataolewa katika jamaa moja ya kabila ya baba yake, ili wana wa Israeli wapate kumiliki kila mtu urithi wa baba zake. 9 Hivyo hapatakuwa na urithi uwao wote utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa kabila za wana wa Israeli zitashikamana kila mmoja na urithi wake mwenyewe. 10 Basi hao binti za Selofehadi wakafanya kama Bwana alivyomwagiza Musa; 11 kwa kuwa Mala, na Tirsa, na Hogla, na Milka, na Noa, binti za Selofehadi waliolewa na waume, wana wa ndugu za baba yao. 12 Waliolewa katika jamaa za wana wa Manase, mwana wa Yusufu, na urithi wao ukakaa katika kabila ya jamaa ya baba yao. 13 Haya ndiyo maagizo na hukumu, ambayo Bwana aliwaagiza wana wa Israeli, kwa mkono wa Musa, hapo katika nchi tambarare za Moabu, karibu na Yordani, hapo Yeriko

Kumbukumbu la Torati 1

1 Haya ndiyo maneno Musa aliyowaambia Israeli wote ng'ambo ya Yordani barani, katika Araba lililoelekea Sufu, kati ya Parani, na Tofeli, na Labani, na Hazerothi, na Dizahabu. 2 Ni mwendo wa siku kumi na moja kutoka Horebu kwa njia ya mlima wa Seiri mpaka Kadesh-barnea. 3 Ikawa mwaka wa arobaini, mwezi wa kumi na moja, siku ya kwanza ya mwezi, Musa akawaambia wana wa Israeli kama yote aliyopewa na Bwana ya kuwaamuru; 4 alipokwisha kumpiga Sihoni mfalme wa Waamori, aliyekuwa akikaa Heshboni, na Ogu mfalme wa Bashani, aliyekuwa akikaa Ashtarothi iliyo katika Edrei; 5 ni ng'ambo ya Yordani katika nchi ya Moabu, alipoanza Musa kufunua torati hii, akisema, 6 Bwana, Mungu wetu, alituambia huko Horebu, akasema, Mlivyokaa katika mlima huu vyatosha; 7 geukeni mshike safari yenu mwende nchi ya milima ya Waamori, na mahali pote palipo karibu ya hapo, katika hiyo Araba, na nchi ya vilima-vilima, na huko Shefela, na Negebu, na pwani-pwani, nchi ya Wakanaani, na Lebanoni, mpaka mto huo mkubwa, mto wa Frati. 8 Angalieni, nimewawekea nchi mbele yenu, ingieni mkaimiliki nchi Bwana aliyowaapia baba zenu, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kwamba atawapa na uzao wao baada yao. 9 Nami wakati ule niliwaambia, nikasema, Siwezi mimi mwenyewe kuwachukua peke yangu. 10 Bwana, Mungu wenu, amewafanya kuwa wengi, nanyi, angalieni, mmekuwa leo mfano wa nyota za mbinguni kwa wingi. 11 Bwana, Mungu wa baba zenu, na awafanye kuwa wengi mara elfu kuliko mlivyo, na kuwabarikia, kama alivyowaahidi. 12 Nitachukuaje peke yangu mimi mwenyewe udhia wenu, na mzigo wenu, na mateto yenu? 13 Jitwalieni watu wenye akili na fahamu, watu wanaojulikana, kwa kadiri ya kabila zenu, nami nitawafanya wawe vichwa juu yenu. 14 Nanyi mkanijibu, mkaniambia, Jambo ulilonena ni jema la kufanya. 15 Basi nikatwaa vichwa vya kabila zenu wenye akili, waliojulikana, nikawafanya wawe vichwa juu yenu, maakida ya elfu elfu, na maakida ya mia mia, na maakida ya hamsini hamsini, na maakida ya kumi kumi, na wenye amri, kwa kadiri ya kabila zenu. 16 Nikawaagiza wakati ule waamuzi wenu, nikawaambia, Sikizeni ninyi maneno kati ya ndugu zenu, mkaamue kwa haki kati ya mtu na nduguye, na mgeni aliye pamoja naye. 17 Msitazame nafsi za watu katika hukumu; mwasikize wadogo na wakubwa sawasawa; msiche uso wa mtu awaye yote; kwa kuwa hukumu ni ya Mungu; na lile neno liwashindalo mniletee mimi, nami nitalisikiza. 18 Nikawaamuru wakati huo mambo yote yaliyowapasa ninyi kuyafanya. 19 Tukasafiri kutoka Horebu, tukapita katikati ya jangwa lile kubwa la kutisha mliloliona, njia ile ya kuiendea nchi ya vilima vya Waamori, kama Bwana, Mungu wetu, alivyotuamuru, tukafika Kadesh-barnea. 20 Nami nikawaambia, Mmefika nchi ya vilima ya Waamori, anayotupa sisi Bwana, Mungu wetu. 21 Tazama, Bwana, Mungu wako, ameiweka nchi mbele yako; haya panda, itamalaki, kama Bwana, Mungu wa baba zako, alivyokuambia; usiogope wala usifadhaike. 22 Nanyi mkanikaribia kila mmoja wenu, mkasema, Na tupeleke watu mbele yetu, ili watupelelezee nchi na kutuletea habari za njia itupasayo kuipandia, na za miji tutakayoifikia. 23 Neno hili likanipendeza sana; nikatwaa watu kumi na wawili, mtu mmoja wa kila kabila. 24 Nao wakageuka, wakapanda mlimani wakafika bonde la Eshkoli, wakalipeleleza. 25 Wakatwaa baadhi ya matunda ya nchi ile mikononi mwao, wakatuletea huku chini, wakatuletea habari tena, wakasema, Nchi hii anayotupa Bwana, Mungu wetu, ni nchi njema. 26 Lakini hamkukubali kukwea huko, mlihalifu neno la Bwana, Mungu wenu; 27 mkanung'unika hemani mwenu, mkasema, Ni kwa sababu Bwana ametuchukia, ndipo akatutoa katika nchi ya Misri, apate kututia katika mikono ya Waamori, ili kutuangamiza. 28 Twakwea kwenda wapi? Ndugu zetu wameiyeyusha mioyo yetu, wakituambia, Wale watu ni wengi, ni warefu kuliko sisi; miji nayo ni mikubwa, imejengewa kuta hata mbinguni; na zaidi ya hayo huko tumewaona Waanaki. 29 Ndipo nikawaambieni, Msifanye hofu, wala msiwache. 30 Bwana, Mungu wenu, anayetangulia mbele yenu, ndiye atakayewapigania, kwa mfano wa yote aliyowafanyia huko Misri mbele ya macho yenu; 31 na huko jangwani, ulipoona alivyokuchukua Bwana, Mungu wako, kama mtu amchukuavyo mwanawe, njia yote mliyoiendea, hata mkafikilia mahali hapa. 32 Lakini katika jambo hili hamkumwamini Bwana, Mungu wenu, 33 aliyewatangulia njiani, usiku kwa moto, kuwaonyesha njia mtakayoiendea, na mchana kwa hilo wingu, ili apate kuwatafutia mahali pa kusimamisha hema zenu. 34 Bwana akaisikia sauti ya maneno yenu, akaghadhibika, akaapa, akasema, 35 Hakika yangu hapana mmoja miongoni mwa watu hawa wa kizazi hiki kibaya atakayeiona nchi hiyo nzuri, niliyowaapia baba zenu kuwapa, 36 isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, huyo ataiona; nami nitampa yeye na watoto wake nchi hiyo aliyoikanyaga; kwa kuwa amemfuata Bwana kwa kila neno. 37 Na Bwana alinikasirikia mimi kwa ajili yenu, akasema, Wala wewe hutaingia humo; 38 Yoshua mwana wa Nuni asimamaye mbele yako ndiye atakayeingia; mtie moyo; kwa kuwa yeye atawarithisha Israeli. 39 Tena, wadogo wenu, mliosema watakuwa mateka, na wana wenu, wasiokuwa leo na maarifa ya mabaya wala mema, ndio watakaoingia, nao ndio nitakaowapa, nao wataimiliki. 40 Na ninyi basi geukeni, mshike safari yenu, mwende jangwani kwa njia ya Bahari ya Shamu. 41 Ndipo mkanijibu, mkaniambia, Sisi tumefanya dhambi juu ya Bwana, tutakwea kupigana kwa mfano wa yote tuliyoamriwa na Bwana. Mkajifunga kila mtu silaha zake za vita, mkafanya wepesi kukwea mlimani. 42 Bwana akaniambia, Uwaambie, Msiende, wala msipigane; kwani mimi si kati yenu; msije mkapigwa mbele ya adui zenu. 43 Basi niliwaambia, msinisikize, bali mliasi amri ya Bwana, mkajikinai, na kukwea mlimani. 44 Na Waamori waliokuwa wakikaa katika mlima huo, waliwatokea juu yenu, wakawafukuza, kama wafukuzwao na nyuki, wakawapomoshea Seiri mpaka Horma. 45 Mkarudi mkalia mbele za Bwana; Bwana asiisikize sauti yenu, wala hakuelekeza masikio yake kwenu. 46 Ndipo mkakaa Kadeshi siku nyingi, kwa kadiri ya hizo siku mlizokaa.

Kumbukumbu la Torati 2

1 Ndipo tukageuka, tukashika safari yetu kwenda jangwani kwa njia ya Bahari ya Shamu, kama alivyoniambia Bwana; tukawa kuizunguka milima ya Seiri siku nyingi. 2 Bwana akanena, akaniambia, 3 Mlivyouzunguka mlima huu vyatosha; geukeni upande wa kaskazini. 4 Nawe waagize watu, uwaambie, Mtapita kati ya mpaka wa ndugu zenu wana wa watu, uwaambie, Mtapita kati ya mpaka wa ndugu zenu wana wa Esau waketio Seiri; nao watawaogopa; basi jiangalieni nafsi zenu sana; 5 msitete nao; kwa maana sitawapa katika nchi yao kamwe, hata kiasi cha kukanyaga wayo wa mguu; kwa kuwa nimempa Esau milima ya Seiri kuwa milki yake. 6 Nunueni vyakula kwao kwa fedha, mpate kula; na maji nayo nunueni kwao kwa fedha, mpate kunywa. 7 Kwa kuwa Bwana, Mungu wako, amekubarikia katika kazi yote ya mkono wako; amejua ulivyotembea katika jangwa kubwa hili; miaka arobaini hii alikuwa nawe Bwana, Mungu wako; hukukosa kitu. 8 Basi tukapita kando yao ndugu zetu wana wa Esau, waketio Seiri kutoka njia ya Araba, kutoka Elathi na kutoka Esion-geberi. Tukageuka tukapita njia ya bara ya Moabu. 9 Bwana akaniambia, usiwasumbue Wamoabi, wala usishindane nao katika mapigano; kwa kuwa sitakupa katika nchi yake kuimiliki; kwa sababu Ari nimewapa wana wa Lutu kuimiliki. 10 (Walioketi humo hapo kale ni Waemi, nao ni watu wakubwa, wengi, warefu, mfano wa Waanaki; 11 na hawa nao wadhaniwa kuwa majitu kama Waanaki;lakini Wamoabi huwaita Waemi. 12 Na Wahori nao walikuwa wakikaa Seiri hapo kale, lakini wana wa Esau waliwafuata; wakawaangamiza mbele yao, wakakaa badala yao; kama alivyofanya Israeli nchi ya milki yake aliyopewa na Bwana.) 13 Sasa basi ondokeni, mkakivuke kijito cha Zeredi. Nasi tukakivuka kile kijito cha Zeredi. 14 Na siku tulizokuwa tukienda kutoka Kadesh-barnea hata tulipovuka kijito cha Zeredi, zilikuwa ni miaka thelathini na minane; maana, hata walipokwisha kuangamizwa watu wa vita kutoka kati ya marago, kizazi chao chote, kama walivyoapiwa na Bwana. 15 Tena mkono wa Bwana ulikuwa juu yao ili kuwaangamiza, kuwatoa kati ya marago, hata walipokoma. 16 Basi ikawa, walipokwisha angamizwa kwa kufa watu wote wa vita kati ya watu, 17 Bwana aliniambia, akasema, 18 Hivi leo ivuke Ari, mpaka wa Moabu; 19 na utakaposongea kuwaelekea wana wa Amoni, usiwasumbue wana wa Amoni, wala usishindane nao; kwa kuwa sitakupa katika nchi ya hao wana wa Amoni kuwa milki yako; kwa sababu nimewapa wana wa Lutu iwe milki yao. 20 (Nchi hiyo nayo yadhaniwa kuwa ni nchi ya Warefai, hapo kale Warefai walikaa humo; lakini Waamoni huwaita Wazamzumi; 21 nao ni watu wengi, wakubwa, warefu, kama Waanaki; lakini Bwana aliwaangamiza mbele yao; wakawafuata wakakaa badala yao; 22 kama vile alivyowafanyia wana wa Esau, waliokaa Seiri, alipowaangamiza Wahori mbele yao; wakawafuata, wakakaa badala yao hata hivi leo; 23 na Waavi waliokuwa wakikaa katika vijiji mpaka Gaza waliangamizwa na Wakaftori waliotoka Kaftori, na hawa wakakaa badala yao.) 24 Ondokeni, mshike safari yenu, mvuke bonde la Arnoni; tazama, nimemtia Sihoni Mwamori mfalme wa Heshboni mkononi mwako, na nchi yake; anzeni kuimiliki, mshindane naye katika mapigano. 25 Hivi leo nitaanza mimi kutia utisho wako na kuhofiwa kwako juu ya watu walio chini ya mbingu kila mahali, watakaosikia uvumi wako, na kutetemeka, na kuingiwa na uchungu kwa sababu yako. 26 Nikatuma wajumbe kutoka bara ya Kedemothi kwenda kwa Sihoni mfalme wa Heshboni na maneno ya amani, kusema. 27 Nipishe katikati ya nchi yako; nitakwenda kwa njia ya barabara, sitageuka kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto. 28 Nawe uniuzie chakula kwa fedha nile; unipe na maji kwa fedha, ninywe; ila unipishe katikati kwa miguu yangu, hayo tu; 29 kama walivyonifanyia hao wana wa Esau waketio Seiri, na hao Wamoabi waketio Ari; hata nivuke Yordani niingie nchi tupewayo na Bwana, Mungu wetu. 30 Lakini Sihoni mfalme wa Heshboni hakutuacha kupitia kwake; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, alimfanya mgumu roho yake, akamtia ukaidi moyoni mwake, apate mtia mkononi mwako kama alivyo hivi leo. 31 Kisha Bwana akaniambia, Tazama, nimeanza kumtoa Sihoni na nchi yake mbele yako; anza kuimiliki, upate kuirithi nchi yake. 32 Ndipo Sihoni alipotutokea juu yetu yeye na watu wake wote, kupigana huko Yahasa. 33 Bwana, Mungu wetu, akamtoa mbele yetu, tukampiga yeye na wanawe, na watu wake wote. 34 Tukatwaa miji yake yote wakati huo, tukaharibu kabisa kila mji uliokuwa na watu, pamoja na wanawake na wadogo; tusimsaze hata mmoja; 35 ila ng'ombe zao tuliwatwaa kuwa mawindo yetu, pamoja na nyara za miji tuliyoitwaa. 36 Kutoka Aroeri iliyo katika ukingo wa bonde la Arnoni, na huo mji ulio ndani ya bonde, mpaka kufika Gileadi, hapakuwa na mji uliokuwa mrefu kutushinda; Bwana, Mungu wetu, aliiweka wazi yote mbele yetu; ila nchi ya wana wa Amoni hukuisongelea; 37 upande wote wa mto wa Yaboki, na miji ya nchi ile ya milimani, na kila mahali alipotukataza Bwana, Mungu wetu.

Kumbukumbu la Torati 3

1 Ndipo tukageuka, tukakwea njia ya Bashani; na Ogu, mfalme wa Bashani, akatutokea juu yetu, yeye na watu wake wote, kuja kupigana huko Edrei. 2 Bwana akaniambia, Usimwogope; kwa kuwa nimemtia mkononi mwako, yeye na watu wake wote na nchi yake; nawe utamtenda mfano wa ulivyomtenda Sihoni, mfalme wa Waamori, aliyekuwa akikaa Heshboni. 3 Basi Bwana, Mungu wetu, akamtia mikononi mwetu na Ogu mfalme wa Bashani, na watu wake wote; tukampiga, asisaziwe cho chote. 4 Tukatwaa miji yake yote wakati huo; hapakuwa na mji tusiotwaa kwao miji sitini, nchi yote ya Argobu, ndio ufalme wa Ogu ulio katika Bashani. 5 Miji hiyo yote ilikuwa yenye maboma marefu, na malango, na makomeo, pamoja na miji isiyokuwa na maboma, mingi sana. 6 Tukaiharibu kabisa, kama tulivyomfanya huyo Sihoni, mfalme wa Heshboni, kwa kuharibu kabisa kila mji uliokuwa na watu, pamoja na wanawake na watoto. 7 Lakini wanyama wote wa mji, na nyara za miji, tulitwaa kuwa mawindo yetu. 8 Tukaitwaa na nchi wakati huo, katika mikono ya hao wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ng'ambo ya Yordani, tokea bonde la Arnoni mpaka kilima cha Hermoni; 9 (na hiyo Hermoni Wasidoni huiita Sirioni, na Waamori huiita Seniri); 10 miji yote ya nchi tambarare, na Gileadi yote, na Bashani yote, mpaka Saleka na Edrei, nayo ni miji ya ufalme wa Ogu katika Bashani. 11 (Kwani aliyesalia katika mabaki ya Warefai ni Ogu pekee, mfalme wa Bashani; tazama, kitanda chake kilikuwa kitanda cha chuma; kitanda hicho je! Hakiko Raba kwa wana wa Amoni? Urefu wake ulikuwa ni mikono kenda,na upana wake mikono minne,kwa mfano wa mkono wa mtu) 12 Na nchi hiyo tuliitwaa ikawa milki yetu, wakati huo; tokea Aroeri iliyo kwenye bonde la Arnoni, na nusu ya nchi ya milima ya Gileadi, na miji iliyokuwamo, niliwapa Wareubeni na Wagadi; 13 na nchi ya Gileadi iliyobaki, na Bashani yote, maana huo ufalme wa Ogu niliwapa nusu ya kabila ya Manase; nchi yote ya Argobu, nayo ndiyo Bashani yote. (Na nchi hii yaitwa nchi ya Warefai. 14 Yairi, mwana wa Manase, alitwaa nchi yote ya Argobu, hata mpaka wa Wageshuri na Wamaaka; akaziita nchi hizo Hawoth-yairi, kwa jina lake mwenyewe, hata hivi leo, maana, hizo nchi za Bashani.) 15 Na Makiri nilimpa Gileadi. 16 Na Wareubeni na Wagadi niliwapa tokea Gileadi mpaka bonde la Arnoni, katikati ya bonde, na mpaka wake; mpaka mto wa Yaboki, nao ni mpaka wa wana wa Amoni; 17 na nchi ya Araba nayo, na mto wa Yordani, na mpaka wake, tokea Kinerethi mpaka bahari ya hiyo Araba, nayo ni Bahari ya Chumvi, chini ya matelemko ya Pisga, upande wa mashariki. 18 Nikawaamuru wakati huo, nikawaambia, Bwana, Mungu wenu, amewapa ninyi nchi hii mwimiliki, basi vukeni ng'ambo wenye silaha mbele ya ndugu zenu, wana wa Israeli, nyote mlio mashujaa. 19 Lakini wake wenu na watoto wenu, na wanyama wenu wa mji, (nawajua kwamba mna wanyama wengi), na wakae katika miji yenu niliyowapa; 20 hata Bwana awapumzishe ndugu zenu kama ninyi, nao pia waimiliki nchi wapewayo na Bwana, Mungu wenu, ng'ambo ya Yordani; ndipo mtakaporudi kila mmoja aende katika milki yake niliyowapa. 21 Nikamwamuru Yoshua wakati huo, nikamwambia, Macho yako yameona yote aliyowatenda Bwana, Mungu wenu, wale wafalme wawili, navyo ndivyo atakavyoutenda Bwana kila ufalme huko uvukiako. 22 Msiwache, kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye awapiganiaye. 23 Nikamnyenyekea Bwana wakati huo, nikamwambia, 24 Ee Bwana Mungu, umeanza kumwonyesha mtumishi wako ukubwa wako, na mkono wako wa nguvu; kwani kuna mungu gani mbinguni au duniani awezaye kufanya mfano wa kazi zako, na mfano wa matendo yako yenye nguvu? 25 Nami nakuomba nivuke, nikaione hiyo nchi nzuri iliyoko ng'ambo ya Jordani, mlima ule mzuri, na Lebanoni. 26 Lakini Bwana alikuwa amenikasirikia kwa ajili yenu, asinisikize; Bwana akaniambia, Na ikutoshe, usinene nami zaidi jambo hili. 27 Kwea katika kilele cha Pisga ukainue macho yako upande wa magharibi, na kaskazini, na kusini, na mashariki, ukatazame kwa macho yako, kwa maana huuvuki mto huu wa Yordani. 28 Lakini mwagize Yoshua umtie moyo mkuu, umtie na nguvu; kwani ndiye atakayevuka mbele ya watu hawa, na nchi utakayoiona atawarithisha yeye. 29 Basi tukakaa katika bonde lililoelekea Beth-peori.

Kumbukumbu la Torati 4

1 Na sasa, Ee Israeli, zisikilizeni amri na hukumu niwafundishazo, ili mzitende; mpate kuishi na kuingia na kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wa baba zenu. 2 Msiliongeze neno niwaamurulo wala msilipunguze, mpate kuzishika amri za Bwana, Mungu wenu, niwaamuruzo. 3 Macho yenu yameona aliyoyatenda Bwana kwa sababu ya Baal-peori; maana wote waliomfuata Baal-peori, Bwana, Mungu wako, amewaangamiza kutoka kati yako. 4 Bali ninyi mlioambatana na Bwana, Mungu wenu, mnaishi kila mmoja wenu, hata leo. 5 Angalieni nimewafundisha amri na hukumu, vile vile kama Bwana, Mungu wangu, alivyoniamuru, ili mzitende katika nchi mwingiayo ili kuimiliki. 6 Zishikeni basi, mkazitende, maana hii ndiyo hekima yenu na akili zenu, machoni pa mataifa watakaozisikia amri hizi zote, nao watasema, Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na akili. 7 Kwa maana liko taifa gani kubwa, lililo na Mungu aliye karibu nao, kama Bwana, Mungu wetu, alivyo, kila tumwitapo? 8 Tena liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo. 9 Lakini, jihadhari nafsi yako, ukailinde roho yako kwa bidii, usije ukayasahau mambo yale uliyoyaona kwa macho yako, yakaondoka moyoni mwako siku zote za maisha yako; bali uwajulishe watoto wako na watoto wa watoto wako; 10 siku ile uliyosimama mbele za Bwana wako huko Horebu, Bwana aliponiambia, Nikusanyieni watu hawa, nami nitawasikizisha maneno yangu, ili wajifunze kunicha mimi siku zote watakazoishi duniani, wakapate na kuwafundisha watoto wao. 11 Mkakaribia, mkasimama chini ya ule mlima; mlima ukawaka moto mpaka kati ya mbinguni, kwa giza na mawingu, na giza kuu. 12 Bwana akasema nanyi kutoka kati ya moto; mkasikia sauti ya maneno, lakini hamkuona umbo lo lote; sauti tu. 13 Akawahubiri agano lake, alilowaamuru kulitenda, yaani, zile amri kumi; akaziandika juu ya mbao mbili za mawe. 14 Bwana akaniamuru wakati ule niwafundishe maagizo na hukumu, mpate kuzitenda katika nchi ile mtakayoivukia ili kuimiliki. 15 Jihadharini nafsi zenu basi; maana hamkuona umbo la namna yo yote siku ile Bwana aliyosema nanyi kutoka kati ya moto; 16 msije mkajiharibu nafsi zenu, mkajifanyia sanamu ya kuchonga, mfano wa sura yo yote, mfano wa mwanamume au mwanamke, 17 mfano wa mnyama ye yote aliye duniani, au mfano wa ndege ye yote arukaye mbinguni, 18 au mfano wa kitu cho chote kitambaacho juu ya ardhi, au mfano wa samaki ye yote aliye majini chini ya nchi; 19 tena usije ukainua macho yako hata mbinguni, na ulionapo jua, na mwezi, na nyota, jeshi la mbinguni lote pia, ukashawishwa na kuviabudu, na kuvitumikia, ambavyo Bwana, Mungu wako amewagawanyia watu wote chini ya mbingu zote. 20 Bali Bwana amewatwaa ninyi, na kuwatoa katika tanuu ya chuma, katika Misri, mpate kuwa watu wa urithi kwake, kama mlivyo leo hivi. 21 Tena Bwana alinikasirikia kwa ajili yenu, akaapa ya kwamba sitavuka Yordani, na ya kwamba sitaingia nchi ile njema, awapayo Bwana, Mungu wenu, iwe urithi. 22 Lakini mimi nitakufa katika nchi hii, sina ruhusa kuvuka Yordani; bali ninyi mtavuka, na kuimiliki nchi ile njema. 23 Jihadharini nafsi zenu, msije mkalisahau agano la Bwana, Mungu wenu, alilolifanya nanyi, mkajifanyia sanamu ya kuchonga, mfano wa umbo la kitu cho chote ulichokatazwa na Bwana, Mungu wenu, 24 kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, ni moto ulao, Mungu mwenye wivu. 25 Utakapozaa wana, na wana wa wana, mkisha kuwa katika nchi siku nyingi, mkajiharibu na kufanya sanamu ya kuchonga kwa umbo la kitu cho chote, mkafanya ambayo ni maovu machoni pa Bwana, Mungu wako, na kumtia hasira; 26 nawashuhudizia mbingu na nchi hivi leo, kwamba karibu mtaangamia kabisa juu ya nchi mwivukiayo Yordani kuimiliki, hamtafanya siku zenu ziwe nyingi juu yake, ila mtaangamizwa kabisa. 27 Na Bwana atawatawanya kati ya mataifa, nanyi mtasalia watu kidogo hesabu yenu kati ya makabila, mtakakopelekwa mbali na Bwana. 28 Na huko mtatumikia miungu, kazi za mikono ya watu, miti na mawe, ambao hawaoni, wala hawasikii, hawali, wala hawanusi. 29 Lakini huko, kama mkimtafuta Bwana, Mungu wako, utampata, ukimtafuta kwa moyo wako wote, na roho yako yote. 30 Na wakati uwapo katika mashaka, ukiisha kupatwa na mambo haya yote, siku za mwisho, utamrudia Bwana, Mungu wako, na kuisikiza sauti yake; 31 kwa kuwa Bwana, Mungu wako, ni Mungu wa rehema; hatakukosa wala kukuangamiza, wala hatalisahau agano la baba zako alilowaapia. 32 Maana uliza sasa siku zilizopita, zilizokuwa kabla yako, tangu siku ile Mungu aliyoumba mwanadamu juu ya nchi, na toka pembe hii ya mbingu hata pembe hii, kwamba kumetukia neno lo lote kama neno hili kubwa, au kwamba kumesikiwa habari ya neno kama hili? 33 Je! Watu wakati wo wote wameisikia sauti ya Mungu ikinena toka kati ya moto, kama wewe ulivyosikia, wasife? 34 Au Mungu amekwenda wakati gani akajitwalia taifa toka kati ya taifa lingine, kwa majaribu, na kwa ishara, na kwa maajabu, na kwa vita, na kwa mkono hodari, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa maogofya makuu, kama vile Bwana, Mungu wenu, alivyowatendea ninyi katika Misri, mbele ya macho yenu? 35 Wewe umeonyeshwa haya, ili upate kujua ya kuwa Bwana ndiye Mungu, hapana mwingine ila yeye. 36 Kutoka mbinguni amekusikizisha sauti yake, ili akufundishe; na juu ya nchi alikuonyesha moto wake mkuu; ukasikia maneno yake toka kati ya moto. 37 Na kwa sababu aliwapenda baba zenu, kwa sababu hiyo aliwachagua wazao wao baada yao, akakutoa katika Misri kwa kuwako pamoja nawe, kwa uweza wake mwingi, 38 ili kufukuza mbele yako mataifa, walio wakubwa, wenye nguvu kukupita wewe, ili kukuingiza, na kukupa nchi yao iwe urithi, kama ilivyo leo. 39 Kwa hiyo ujue, leo hivi, ukaweke moyoni mwako, ya kuwa Bwana ndiye Mungu katika mbingu juu, na katika nchi chini; hapana mwingine. 40 Basi, zishike sheria zake, na amri zake, ninazokuamuru leo, upate kufanikiwa, wewe na watoto wako baada yako, na siku zako ziwe nyingi katika nchi ile akupayo Bwana, Mungu wako, milele. 41 Ndipo Musa akabagua miji mitatu ng'ambo ya Yordani upande wa matokeo ya jua; 42 ili kwamba amwuaye mtu apate kukimbilia huko, amwuaye jirani yake pasipo kujua, wala hakumchukia tangu hapo; ili apate kuishi akimbiliapo mmojawapo miji hiyo; 43 nayo ni hii, Beseri ya barani iliyo katika nchi tambarare, kwa Wareubeni; na Ramothi iliyo Gileadi, kwa Wagadi; na Golani iliyo Bashani, kwa Wamanase. 44 Na torati Musa aliyowawekea wana wa Israeli ni hii; 45 haya ndiyo mashuhudizo, na amri, na hukumu, Musa alizowaambia wana wa Israeli walipotoka Misri; 46 ng'ambo ya Yordani, katika bonde lililoelekea Beth-peori, katika nchi ya Sihoni mfalme wa Waamori, aliyekuwa akikaa Heshboni ndiye aliyepigwa na Musa na wana wa Israeli, walipotoka Misri; 47 wakaishika nchi yake, ikawa milki yao, na nchi ya Ogu mfalme wa Bashani, ndio wafalme wawili wa Waamori, waliokuwa ng'ambo ya Yordani upande wa matokeo ya jua; 48 toka Aroeri, iliyo juu ya ukingoni pa bonde la Arnoni, hata mpaka mlima wa Sioni (nao ndio Hermoni), 49 na Araba yote iliyo ng'ambo ya Yordani upande wa mashariki, hata mpaka bahari ya Araba, chini ya matelemko ya Pisga.

Kumbukumbu la Torati 5

1 Musa akawaita Israeli wote, akawaambia, Enyi Israeli, zisikieni amri na hukumu ninenazo masikioni mwenu leo, mpate kujifunza na kuangalia kuzitenda. 2 Bwana, Mungu wetu, alifanya agano nasi katika Horebu. 3 Bwana hakufanya agano hili na baba zetu, bali na sisi, yaani, sisi sote tuliopo hapa, tu hai. 4 Bwana alisema nanyi uso kwa uso mlimani, toka kati ya moto; 5 (nami wakati ule nalisimama kati ya Bwana na ninyi, ili kuwaonyesha neno la Bwana; maana, mliogopa kwa sababu ya ule moto, wala hamkupanda mlimani); naye akasema, 6 Mimi ni Bwana, Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa. 7 Usiwe na miungu mingine ila mimi. 8 Usijifanyie sanamu ya kuchonga, mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, au kilicho chini duniani, au kilicho majini chini ya nchi. 9 Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi Bwana, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu, nawapatiliza wana uovu wa baba zao; hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao, 10 nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu. 11 Usilitaje bure Jina la Bwana, Mungu wako; maana Bwana hatamhesabia kuwa hana hatia, mtu alitajaye jina lake bure. 12 Ishike siku ya Sabato uitakase, kama Bwana, Mungu wako, alivyokuamuru. 13 Siku sita fanya kazi, utende mambo yako yote; 14 lakini siku ya saba ni Sabato ya Bwana, Mungu wako; siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe, wala mwanao, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala ng'ombe wako, wala punda wako, wala mnyama wako ye yote, wala mgeni aliye ndani ya malango yako, ili mtumwa wako na mjakazi wako wapumzike vile vile kama wewe. 15 Nawe utakumbuka ya kuwa wewe ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri, na ya kuwa Bwana, Mungu wako, alikutoa huko kwa mkono wenye nguvu, na mkono ulionyoshwa; kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wako, alikuamuru uishike sabato. 16 Waheshimu baba yako na mama yako; kama Bwana, Mungu wako, alivyokuamuru, siku zako zipate kuzidi, nawe upate kufanikiwa katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako. 17 Usiue. 18 Wala usizini. 19 Wala usiibe. 20 Wala usimshuhudie jirani yako uongo. 21 Wala usimtamani mke wa jirani yako; wala usiitamani nyumba ya jirani yako, wala shamba lake, wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng'ombe wake, wala punda wake, wala kitu cho chote alicho nacho jirani yako. 22 Haya ndiyo maneno ambayo Bwana aliwaambia mkutano wenu wote mlimani kwa sauti kuu toka kati ya moto, na wingu, na giza kuu; wala hakuongeza neno. Akayaandika juu ya mbao mbili za mawe, akanipa. 23 Ikawa, mlipoisikia sauti ile toka kati ya giza, na wakati uo huo mlima ule ulikuwa ukiwaka moto, basi, mlinikaribia, naam, wakuu wote wa kabila zenu, na wazee wenu, 24 mkasema, Tazama, Bwana, Mungu wetu, ametuonyesha utukufu wake, na ukuu wake, nasi tunasikia sauti yake toka kati ya moto; mmeona leo ya kuwa Mungu husema na mwanadamu, naye akaishi. 25 Sasa basi, mbona tufe? Maana moto huu mkubwa utatuteketeza; tukiisikia tena sauti ya Bwana, Mungu wetu, tutakufa. 26 Maana katika wote wenye mwili ni nani aliyeisikia sauti ya Mungu aliye hai, akisema toka kati ya moto, kama vile sisi, asife? 27 Enenda karibu wewe, ukasikie yote atakayoyasema Bwana, Mungu wetu; ukatuambie yote atakayokuambia Bwana, Mungu wetu; nasi tutayasikia na kuyatenda. 28 Naye Bwana akasikia sauti ya maneno yenu mliyoniambia; Bwana akaniambia, Nimesikia sauti ya maneno ya watu hawa waliyokuambia; wamesema vema yote waliyosema. 29 Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha, na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele! 30 Enda uwaambie, Rudini hemani mwenu. 31 Lakini wewe, simama hapa karibu nami, nami nitanena nawe sheria zote, na amri na hukumu, utakazowafunza, wapate kuzifanya katika nchi niwapayo kuimiliki. 32 Tunzeni basi, mtende kama mlivyoamriwa na Bwana, Mungu wenu; msikengeuke kwa mkono wa kuume wala wa kushoto. 33 Endeni njia yote aliyowaagiza Bwana, Mungu wenu, mpate kuwa hai, na kufanikiwa, mkafanye siku zenu kuwa nyingi katika nchi mtakayoimiliki.

Kumbukumbu la Torati 6

1 Na hii ndiyo sheria, na amri, na hukumu, alizoziamuru Bwana, Mungu wenu, mfundishwe, mpate kuzitenda katika nchi ile mnayoivukia kuimiliki; 2 upate kumcha Bwana, Mungu wako, kushika amri zake zote, na sheria zake, ninazokuamuru, wewe na mwanao, na mwana wa mwanao, siku zote za maisha yako; tena siku zako ziongezwe. 3 Sikiza basi, Ee Israeli, ukaangalie kuzitenda; upate kufanikiwa, mpate kuongezeka sana, kama Bwana, Mungu wa baba zako, alivyokuahidi, katika nchi ijaayo maziwa na asali. 4 Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. 5 Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. 6 Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; 7 nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. 8 Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako. 9 Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako. 10 Tena itakuwa atakapokwisha Bwana, Mungu wako, kukuleta katika nchi aliyowaapia babu zako, Ibrahimu na Isaka na Yakobo, ya kuwa atakupa; miji mikubwa mizuri usiyoijenga wewe, 11 na nyumba zimejaa vitu vyema vyote usizojaza wewe, na visima vimefukuliwa usivyofukua wewe, mashamba ya mizabibu na mizeituni usiyoipanda wewe, nawe utakula na kushiba; 12 ndipo ujitunze, usije ukamsahau Bwana aliyekutoa nchi ya Misri, nyumba ya utumwa. 13 Mche Bwana, Mungu wako; ndiye utakayemtumikia, na kuapa kwa jina lake. 14 Msifuate miungu mingine katika miungu ya mataifa wawazungukao; 15 kwani Bwana, Mungu wako, aliye katikati yako ni Mungu mwenye wivu; isije ikawaka juu yako hasira ya Bwana, Mungu wako, akakuangamiza kutoka juu ya uso wa nchi. 16 Msimjaribu Bwana, Mungu wenu, kama mlivyomjaribu huko Masa. 17 Zishikeni kwa bidii sheria za Bwana, Mungu wenu, na mashuhudizo yake, na amri zake alizokuagiza. 18 Nawe fanya yaliyo sawa, na mema, machoni pa Bwana; ili mpate kufanikiwa, nawe upate kuingia na kuimiliki nchi nzuri Bwana aliyowaapia baba zako, 19 ya kuwa atawasukumia nje adui zako wote mbele yako, kama alivyosema Bwana. 20 Na zamani zijazo atakapokuuliza mwanao, akikuambia, N'nini mashuhudizo, na amri, na hukumu, alizowaagiza Bwana, Mungu wetu? 21 Ndipo umwambie mwanao, Tulikuwa watumwa wa Farao huko Misri; Bwana, akatutoa kutoka Misri kwa mkono wa nguvu; 22 Bwana akaonya ishara na maajabu, makubwa, mazito, juu ya Misri, na juu ya Farao, na juu ya nyumba yake yote, mbele ya macho yetu; 23 akatutoa huko ili kututia huku, apate kutupa nchi aliyowaapia baba zetu. 24 Bwana akatuamuru kuzifanya amri hizi zote, tumche Bwana, Mungu wetu, tuone mema sikuzote ili atuhifadhi hai kama hivi leo. 25 Tena itakuwa haki kwetu, tukitunza kufanya maagizo haya yote mbele ya Bwana, Mungu wetu, kama alivyotuagiza.

Kumbukumbu la Torati 7

1 Bwana, Mungu wako, atakapokutia katika nchi uendayo kuimiliki, atakapoyang'oa mataifa mengi watoke mbele yako, Mhiti, na Mgirgashi, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, mataifa saba makubwa yenye nguvu kukupita wewe; 2 wakati Bwana, Mungu wako, atakapowatoa mbele yako, nawe utawapiga; wakati huo ndipo uwaondoe kabisa; usifanye agano nao, wala kuwahurumia; wala usioane nao; 3 binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake. 4 Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine; ndipo itakapowaka hasira ya Bwana juu yenu, naye atakuangamiza upesi. 5 Lakini watendeni hivi; zivunjeni madhabahu zao zibomosheni nguzo zao, yakateni maashera yao, ziteketezeni kwa moto sanamu zao za kuchonga. 6 Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako; Bwana Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi. 7 Bwana hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; 8 bali kwa sababu Bwana anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu Bwana akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa, katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri. 9 Basi jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu; 10 naye huwalipa wamchukiao mbele ya uso wao, kuwaangamiza. Hatakuwa mlegevu kwake yeye amchukiaye, atamlipa mbele ya uso wake. 11 Basi zishike amri, na sheria, na hukumu ninazokuamuru leo, uzitende. 12 Na itakuwa, kwa sababu mwazisikiliza hukumu hizi, na kuzishika na kuzitenda, basi Bwana, Mungu wako, atakutimilizia agano na rehema aliyowaapia baba zako; 13 naye atakupenda na kukubarikia na kukuongeza tena ataubarikia uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, nafaka zako na divai yako, na mafuta yako, maongeo ya ng'ombe zako, na wadogo wa kondoo zako, katika nchi aliyowaapia baba zako kuwa atakupa. 14 Utabarikiwa kuliko mataifa yote; hakutakuwa na mtu mume wala mke aliye tasa kati yenu; wala kati ya wanyama wenu wa mifugo. 15 Na Bwana atakuondolea ugonjwa wote; wala hatatia juu yako maradhi yo yote mabaya uyajuayo ya Misri, lakini atayaweka juu ya wote wakuchukiao. 16 Nawe angamiza mataifa yote atakayokupa Bwana, Mungu wako; jicho lako lisiwahurumie, wala usiitumikie miungu yao; kwani litakuwa ni mtego kwako jambo hilo. 17 Nawe kama ukisema moyoni mwako, Mataifa haya ni mengi kunipita mimi; nitawatoaje katika milki yao? 18 Usiwaogope; kumbuka sana Bwana, Mungu wako, alivyomfanya Farao na Misri yote; 19 uyakumbuke hayo majaribu makuu yaliyoyaona macho yako, na hizo ishara, na maajabu, na mkono wa nguvu, na mkono ulionyoka, aliokutolea nje Bwana, Mungu wako; ndivyo atakavyowafanya Bwana, Mungu wako, mataifa yote unaowaogopa. 20 Tena Bwana, Mungu wako, atampeleka mavu kati yao, hata hao watakaosalia, hao wajifichao, waangamie mbele zako. 21 Usiingiwe na kicho kwa sababu yao; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu katikati yako, Mungu mkuu, mwenye utisho. 22 Naye Bwana, Mungu wako, atayatupia nje mataifa yale mbele yako kidogo kidogo; haikupasi kuwaangamiza kwa mara moja, wasije wakaongezeka kwako wanyama wa mwitu. 23 Ila Bwana, Mungu wako, atawatoa mbele yako, atawatia mashaka, mashaka makuu, hata waishe kuangamizwa. 24 Na wafalme wao atakutilia mkononi mwako, nawe utalipoteza jina lao litoke chini ya mbingu; hapana mtu atakayeweza kusimama mbele yako, hata utakapokwisha kuwaangamiza. 25 Sanamu za kuchonga za miungu yao mtaziteketeza kwa moto; usitamani fedha wala dhahabu iliyo juu yao, wala usiitwae iwe yako usije ukanaswa nayo; kwa maana ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako; 26 na machukizo usitie ndani ya nyumba yako, usije wewe kuwa kitu cha haramu mfano wake; ukichukie kabisa, na kukikataa kabisa; kwa kuwa ni kitu kilichoharimishwa.

Kumbukumbu la Torati 8

1 Amri hii ninayokuamuru leo mtaishika kuitenda, mpate kuishi na kuongezeka, na kuingia katika nchi ile ambayo Bwana aliwaapia baba zenu; nanyi mtaimiliki. 2 Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo. 3 Akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha Bwana. 4 Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arobaini. 5 Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo Bwana, Mungu wako, akurudivyo. 6 Nawe uzishike amri za Bwana, Mungu wako, upate kwenda katika njia zake, na kumcha. 7 Kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yuakuingiza katika nchi nzuri, nchi yenye vijito vya maji, na chemchemi, na visima, vibubujikavyo katika mabonde na milima; 8 nchi ya ngano na shayiri, na mizabibu, na mitini, na mikomamanga; nchi ya mizeituni yenye mafuta, na asali; 9 nchi utakayokula mikate humo, pasina shida, hutapungukiwa na kitu ndani yake; nchi ambayo mawe yake ni chuma, na milima yake yafukuka shaba. 10 Nawe utakula ushibe, utamshukuru Bwana, Mungu wako, kwa nchi nzuri aliyokupa. 11 Jihadhari, usije ukamsahau Bwana, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na sheria zake, ninazokuamuru leo. 12 Angalia, utakapokuwa umekula na kushiba, na kujenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake; 13 na makundi yako ya ng'ombe na kondoo yatakapoongezeka, na fedha yako na dhahabu yako itakapoongezeka, na kila kitu ulicho nacho kitakapoongezeka; 14 basi hapo moyo wako usiinuke, ukamsahau Bwana, Mungu wako, aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa; 15 aliyekuongoza katika jangwa lile kubwa lenye kitisho, lenye nyoka za moto na nge, nchi ya kiu isiyokuwa na maji; aliyekutolea maji katika mwamba mgumu, 16 aliyekulisha jangwani kwa mana, wasiyoijua baba zako; apate kukutweza, apate kukujaribu, ili kukutendea mema mwisho wako. 17 Hapo usiseme moyoni mwako, Nguvu zangu na uwezo wa mkono wangu ndio ulionipatia utajiri huo. 18 Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo. 19 Lakini itakuwa, kama ukimsahau Bwana, Mungu wako, na kuiandama miungu mingine, na kuitumikia na kuiabudu, nawashuhudia leo ya kuwa mtaangamia bila shaka. 20 Kama vile mataifa yale ambayo Bwana anawaangamiza mbele yenu, ndivyo mtakavyoangamia; kwa sababu hamkutaka kuisikiliza sauti ya Bwana, Mungu wenu.

Kumbukumbu la Torati 9

1 Sikiza, Ee Israeli; hivi leo unataka kuvuka Yordani uingie kwa kuwamiliki mataifa yaliyo makubwa, na yenye nguvu kukupita wewe, miji mikubwa iliyojengewa kuta hata mbinguni, 2 watu wakubwa, warefu, wana wa Waanaki, uwajuao, uliokuwa ukisikia wakitajwa hivi, Ni nani awezaye kusimama mbele ya wana wa Anaki? 3 Basi jua siku hii ya leo kuwa Bwana, Mungu wako, ndiye atanguliaye kuvuka mbele yako kama moto uteketezao; atawaangamiza, tena atawaangusha mbele yako; ndivyo utakavyowafukuza na kuwapoteza upesi, kama alivyokuambia Bwana. 4 Usiseme moyoni mwako, Bwana, Mungu wako, atakapokwisha kuwasukumia nje mbele yako, ukasema, Ni kwa haki yangu alivyonitia Bwana niimiliki nchi hii; kwani ni kwa ajili ya uovu wa mataifa haya Bwana awafukuza nje mbele yako. 5 Si kwa haki yako, wala kwa unyofu wa moyo wako, hivi uingiavyo kuimiliki nchi yao; lakini ni kwa uovu wa mataifa haya Bwana, Mungu wako, awafukuza nje mbele yako; tena apate kuliweka imara hilo neno Bwana alilowaapia baba zako Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo. 6 Basi jua ya kuwa Bwana, Mungu wako, hakupi nchi hii nzuri uimiliki kwa ajili ya haki yako, kwa maana u taifa lenye shingo ngumu. 7 Kumbuka, usisahau ulivyomtia Bwana, Mungu wako, kasirani jangwani; tangu siku uliyotoka nchi ya Misri hata mlipofika mahali hapa, mmekuwa na uasi juu ya Bwana 8 Tena mlimkasirisha Bwana katika Horebu, Bwana akakasirika nanyi hata akataka kuwaangamiza. 9 Na hapo nilipokwea mlimani kwenda kuzipokea mbao za mawe, nazo ni mbao za agano Bwana alilofanya nanyi, ndipo nikakaa mle mlimani siku arobaini usiku na mchana; sikula chakula wala kunywa maji. 10 Bwana akanipa zile mbao mbili za mawe zimeandikwa kwa kidole cha Mungu; na juu yake yameandikwa maneno mfano wa yote aliyosema nanyi Bwana mle mlimani toka kati ya moto siku ya mkutano. 11 Ikawa mwisho wa siku arobaini usiku na mchana, Bwana alinipa zile mbao mbili za mawe, nazo ni mbao za agano. 12 Bwana akaniambia, Ondoka huko, shuka upesi; kwa kuwa watu wako uliowatoa Misri wamejiharibu; wamekengeuka mara katika njia niliyowaamuru; wamejifanyia sanamu ya kusubu. 13 Tena Bwana akasema nami zaidi, akaniambia, Nimeliona taifa hili; na tazama, ni taifa lenye shingo ngumu; 14 niache, nipate kuwaangamiza, na kulifuta jina lao chini ya mbingu; nami nitakufanya wewe uwe taifa kubwa lenye nguvu kuwapita wao. 15 Basi nikageuka nikashuka mle mlimani, mlima ukawaka moto; na zile mbao mbili za agano zilikuwa katika mikono yangu miwili. 16 Nikaangalia, na tazama, mlikuwa mmefanya dhambi juu ya Bwana, Mungu wenu; mmefanya ndama ya ng'ombe ya kusubu; mmekengeuka upesi katika njia aliyowaamuru Bwana. 17 Nikazishika zile mbao mbili, nikazitupa kutoka katika mikono yangu miwili, nikazivunja mbele ya macho yenu. 18 Nikaanguka nchi mbele za Bwana siku arobaini usiku na mchana, kama pale kwanza; sikula chakula wala kunywa maji; kwa sababu ya makosa yenu yote mliyokosa, kwa kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, kwa kumkasirisha. 19 Kwa kuwa niliogopa hasira na makamio aliyowakasirikia Bwana kutaka kuwaangamiza. Lakini Bwana alinisikiza wakati huo nao. 20 Bwana akamkasirikia sana Haruni akataka kumwangamiza; nikamwombea Haruni naye wakati huo. 21 Kisha nikaitwaa ile dhambi yenu, huyo ndama mliyemfanya, nikamteketeza kwa moto, nikamponda, nikamsaga tikitiki, hata akawa laini kama vumbi; nikalitupa vumbi lake katika kijito kilichoshuka kutoka mlimani. 22 Tena huko Tabera, na Masa, na Kibroth-hataava mlimtia Bwana hasira. 23 Na wakati alipowatuma Bwana kutoka Kadesh-barnea, akiwaambia, Kweeni mkaimiliki nchi niliyowapa; ndipo mkaasi juu ya maagizo ya Bwana, Mungu wenu, hamkumsadiki wala hamkusikiza sauti yake. 24 Mmekuwa na uasi juu ya Bwana tokea siku nilipowajua ninyi. 25 Ndipo nikaanguka nchi mbele za Bwana siku zile arobaini usiku na mchana nilizokuwa nimeanguka nchi; kwa kuwa Bwana alisema atawaangamiza. 26 Nikamwomba Bwana, nikasema, Ee Bwana Mungu, usiwaangamize watu wako, urithi wako, uliowakomboa kwa ukuu wako, uliowatoa Misri kwa mkono wa nguvu. 27 Wakumbuke watumwa wako, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo; usiangalie upotofu wa watu hawa, wala uovu wao, wala dhambi yao; 28 isije nchi uliyotutoa ikasema, Ni kwa sababu Bwana hakuweza kuwaleta katika nchi aliyowapa ahadi, tena ni kwa kuwa aliwachukia, alivyowatoa nje ili kuwaua jangwani. 29 Nao ni watu wako, urithi wako, uliowatoa kwa nguvu zako kuu na mkono wako ulionyoka.

Kumbukumbu la Torati 10

1 Wakati ule Bwana akaniambia, Chonga mbao mbili za mawe mfano wa zile za kwanza, kisha uje kwangu huku mlimani, ukajifanyie na sanduku la mti. 2 Nami nitaandika juu ya hizo mbao maneno hayo yaliyokuwa juu ya mbao za kwanza, ulizozivunja, nawe uzitie ndani ya hilo sanduku. 3 Basi nikafanya sanduku la mti wa mshita, nikachonga mbao mbili za mawe mfano wa zile za kwanza, nikakwea mle mlimani, na zile mbao mbili mkononi mwangu. 4 Naye akaandika juu ya mbao mfano wa maandiko ya kwanza, zile amri kumi, alizowaambia Bwana huko mlimani toka kati ya moto siku ya mkutano; Bwana akanipa. 5 Basi nikageuka nikashuka kutoka mlimani, nikazitia mbao ndani ya sanduku nililofanya; nazo zimo humo kama alivyoniamuru Bwana. 6 (Wana wa Israeli wakasafiri kutoka visima vya Bene-Yaakani kwenda Mosera; Haruni akafa huko, akazikwa huko; na Eleazari mwanawe alitumika utumishi wa ukuhani badala yake. 7 Wakasafiri kutoka huko kwenda Gudgoda; wakatoka Gudgoda wakaenda Yotbatha, nayo ni nchi ya vijito vya maji. 8 Na wakati huo Bwana aliitenga kabila ya Lawi ili walichukue lile sanduku la agano la Bwana, wasimame mbele ya Bwana kwa kumtumikia, na kuwabarikia watu kwa jina lake, hata hivi leo. 9 Ndipo asiwe na fungu Lawi, wala urithi pamoja na nduguze; Bwana ndiye urithi wake, kwa mfano wa vile alivyomwambia Bwana, Mungu wako.) 10 Nikakaa mle mlimani kama hapo kwanza, siku arobaini usiku na mchana; Bwana akanisikiza wakati huo nao; asitake Bwana kukuangamiza. 11 Bwana akaniambia, Ondoka, ushike safari yako mbele ya watu; nao wataingia waimiliki nchi, niliyowaapia baba zao ya kuwa nitawapa. 12 Na sasa, Israeli, Bwana, Mungu wako, anataka nini kwako, ila umche Bwana, Mungu wako, na kwenda katika njia zake zote, na kumpenda, na kumtumikia Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote; 13 kuzishika amri za Bwana na sheria zake, ninazokuamuru leo, upate uheri? 14 Tazama, mbingu ni mali za Bwana, Mungu wako, na mbingu za mbingu, na nchi, na vitu vyote vilivyomo. 15 Tena, Bwana aliwafurahia baba zako, na kuwapenda, akawachagua wazao wao baada yao, naam, na ninyi zaidi ya mataifa yote kama hivi leo. 16 Basi, zitahirini govi za mioyo yenu, wala msiwe na shingo ngumu. 17 Kwa maana Bwana, Mungu wenu, yeye ndiye Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, asiyependelea nyuso za watu, wala hakubali rushwa. 18 Huwafanyia yatima na mjane hukumu ya haki, naye humpenda mgeni, akimpa chakula na mavazi. 19 Basi, mpendeni mgeni, kwa sababu ninyi wenyewe mlikuwa wageni katika nchi ya Misri. 20 Mche Bwana, Mungu wako, umtumikie yeye; ambatana naye, na kuapa kwa jina lake. 21 Yeye ndiye fahari yako, na yeye ndiye Mungu wako, aliyekutendea mambo haya makubwa, ya kutisha, uliyoyaona kwa macho yako. 22 Baba zako walishukia Misri na watu sabini; na sasa Bwana, Mungu wako, amekufanya kama nyota za mbinguni kwa wingi.

Kumbukumbu la Torati 11

1 Kwa ajili hii mpende Bwana, Mungu wako, na kushika sikuzote mausia yake, na amri zake, na hukumu zake, na maagizo yake. 2 Nanyi leo jueni; kwa kuwa sisemi sasa na vijana vyenu, ambao hawakujua, wala hawakuona adhabu ya Bwana, Mungu wenu, ukuu wake, na mkono wake wa nguvu, na mkono wake ulionyoka, 3 na ishara zake, na kazi zake alizomfanya Farao mfalme wa Misri, na nchi yake yote, katikati ya Misri; 4 na alivyolifanya jeshi la Misri, farasi zao, na magari yao; na alivyowafunikiza maji ya Bahari ya Shamu walipokuwa wakiwaandamia, na alivyowaangamiza Bwana hata hivi leo; 5 na mambo aliyowafanyia ninyi barani, hata mkaja mahali hapa; 6 na alivyowafanya Dathani, na Abiramu, wana wa Eliabu mwana wa Reubeni; nchi ilivyofunua kinywa chake, ikawameza, na walio nyumbani mwao, na mahema yao, na kila kitu kilichokuwa hai kikiwafuata, katikati ya Israeli yote; 7 lakini macho yenu yameiona kazi kubwa ya Bwana aliyoifanya, yote. 8 Kwa hiyo yaangalieni maagizo yote niwaagizayo leo, mpate kuwa na nguvu, na kuingia mkaimiliki nchi mwivukiayo kuimiliki; 9 nanyi mpate kuzifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi Bwana aliyowaapia baba zenu, ya kuwa atawapa wao na kizazi chao, nchi imiminikayo maziwa na asali 10 Kwa kuwa nchi mwingiayo kuimiliki, si mfano wa nchi ya Misri mlikotoka, uliyokuwa ukipanda mbegu zako humo na kuinywesheleza kwa mguu wako, kama shamba la mboga; 11 lakini nchi mwivukiayo kuimiliki ni nchi ya vilima na mabonde, nayo hunyweshwa maji ya mvua ya mbinguni; 12 nayo ni nchi itunzwayo na Bwana, Mungu wako; macho ya Bwana Mungu wako, ya juu yake, tangu mwanzo wa mwaka hata mwisho wa mwaka. 13 Tena itakuwa, mtakaposikiza kwa bidii maagizo yangu niwaagizayo leo, kwa kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kumtumikia kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote, 14 ndipo nitakapowapa mvua ya nchi yenu kwa wakati wake, mvua ya masika, na mvua ya vuli, upate kuvuna nafaka yako, na divai yako, na mafuta yako. 15 Nami nitakupa nyasi katika mavue yako kulisha wanyama wako wa mifugo, nawe utakula na kushiba. 16 Jitunzeni nafsi zenu, mioyo yenu isije ikadanganywa, mkageuka na kutumikia miungu mingine na kuiabudu; 17 hasira za Bwana zikawaka juu yenu, naye akafunga mbingu kusiwe na mvua, wala nchi isitoe matunda yake; mkaangamia kwa upesi mtoke katika nchi nzuri awapayo Bwana. 18 Kwa hiyo yawekeni maneno yangu mioyoni mwenu na rohoni mwenu; yafungeni yawe dalili juu ya mikono yenu, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yenu. 19 Nayo wafunzeni vijana vyenu kwa kuyazungumza uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. 20 Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako; 21 ili siku zenu zifanywe nyingi, na za vijana vyenu nao, juu ya nchi Bwana aliyowaapia baba zenu kuwa atawapa, kama zilivyo siku za mbingu juu ya nchi. 22 Kwa kuwa kwamba mtayashika kwa bidii maagizo haya yote niwaagizayo, kuyafanya; kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kutembea katika njia zake zote, na kushikamana naye; 23 ndipo Bwana atakapowafukuza mataifa haya yote mbele yenu, nanyi mtamiliki mataifa makubwa yenye nguvu kuwapita ninyi. 24 Kila mahali mtakapokanyaga kwa nyayo za miguu yenu patakuwa penu; tokea hilo jangwa, na Lebanoni, na tokea mto wa Frati, mpaka bahari ya magharibi, itakuwa ndiyo mipaka yenu. 25 Hapatakuwa na mtu atakayeweza kusimama mbele yenu; Bwana, Mungu wenu, ataweka utisho wenu na kuhofiwa kwenu juu ya nchi yote mtakayoikanyaga, kama alivyowaambia. 26 Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana; 27 baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, niwaagizayo leo; 28 na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua. 29 Tena itakuwa, atakapokuleta Bwana, Mungu wako, na kukutia katika nchi uendeayo kuimiliki, ndipo uiweke baraka juu ya mlima wa Gerizimu, na laana uiweke juu ya mlima wa Ebali. 30 Je! Haiwi ng'ambo ya Yordani? Nyuma ya njia ya machweo ya jua, katika nchi ya Wakanaani waketio katika Araba kuelekea Gilgali, kando ya hiyo mialoni ya More? 31 Kwani ninyi mtavuka Yordani mwingie kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wenu, nanyi muimiliki na kuketi humo. 32 Nanyi angalieni mzifanye amri na hukumu zote niwawekeazo leo mbele yenu.

Kumbukumbu la Torati 12

1 Hizi ndizo amri na hukumu mtakazotunza kuzifanya katika nchi aliyokupa Bwana, Mungu wa baba zako, uimiliki, siku zote mtakazoishi juu ya nchi. 2 Vunjeni kabisa mahali pote walipokuwa wakiitumikia miungu yao mataifa mtakayoyamiliki, juu ya milima mirefu, na juu ya vilima, na chini ya kila mti wenye majani mabichi; 3 nanyi zivunjeni madhabahu zao, zibomoeni nguzo zao, na maashera yao yateketezeni kwa moto, na sanamu za kuchonga za miungu yao zikateni; na jina lao lifutilieni mbali na mahali hapo. 4 Wala msimfanyie hivyo Bwana, Mungu wenu. 5 Lakini mahali atakapochagua Bwana, Mungu wenu, katika kabila zenu zote, apaweke jina lake, maana, ni makao yake, elekezeni nyuso zenu hapo, nawe wende huko; 6 pelekeni huko sadaka zenu za kuteketezwa, na dhabihu zenu, na zaka zenu, na sadaka ya kuinuliwa ya mikono yenu, na nadhiri zenu, na sadaka zenu za hiari, na wazaliwa wa kwanza wa makundi yenu ya ng'ombe na ya kondoo; 7 na huko mtakula mbele za Bwana, Mungu wenu, nanyi furahini katika yote mtakayotia mikono yenu, ninyi na wa nyumbani mwenu, aliyokubarikia Bwana, Mungu wako. 8 Msifanye kwa kufuata mambo yote tuyafanyayo hapa leo, kila mtu kama aonavyo vema machoni pake; 9 kwani hamjafikilia bado katika raha na urithi akupao Bwana, Mungu wako. 10 Lakini mtakapovuka Yordani na kukaa katika nchi anayowarithisha Bwana, Mungu wenu, akawapeni raha, akiwaokoa na adui zenu pande zote, mkakaa salama; 11 wakati huo itakuwa kwamba mahali pale atakapopachagua Bwana, Mungu wenu, alikalishe jina lake, hapo ndipo mtakapoleta kila kitu ninachowaamuru; sadaka zenu za kuteketezwa, na dhabihu zenu, na zaka zenu, na sadaka ya kuinuliwa ya mikono yenu, na nadhiri zenu zote teule mtakazoweka kwa Bwana. 12 Nanyi mtafurahi mbele za Bwana, Mungu wenu, ninyi, na wana wenu, na binti zenu, na watumishi wenu wanawaume na wanawake, na Mlawi aliyemo malangoni mwenu; kwa kuwa hana sehemu wala urithi kwenu. 13 Ujihadhari usitoe sadaka zako za kuteketezwa katika kila mahali upaonapo; 14 bali katika mahali atakapopachagua Bwana katika kabila zako mojawapo, ndipo utakapotoa sadaka zako za kuteketezwa, ndipo utakapotenda yote nikuamuruyo. 15 Pamoja na haya waweza kuchinja nyama na kula ndani ya malango yako yote, kwa kufuata yote yatamaniwayo na roho yako, kwa mfano wa baraka ya Bwana, Mungu wako, aliyokupa; aliye tohara na asiye tohara ana ruhusa kula katika nyama hiyo, kama ya paa na ya kulungu. 16 Lakini msiile damu; imwageni juu ya nchi kama maji. 17 Usile ndani ya malango yako zaka ya nafaka zako, wala ya divai yako, wala ya mafuta yako, wala wazaliwa wa kwanza wa makundi yako, ya ng'ombe wala ya kondoo, wala nadhiri zako uwekazo zo zote, wala sadaka zako za hiari, wala sadaka ya kuinuliwa ya mkono wako; 18 lakini hivyo mtakula mbele za Bwana, Mungu wako, mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako, wewe, na mwanao mume na mke, na mtumwa wako mume na mke, na Mlawi aliye ndani ya malango yako; nawe furahi mbele za Bwana, Mungu wako, katika yote utakayotia mkono wako. 19 Jilinde nafsi yako usimwache Mlawi siku zote uishizo katika nchi yako. 20 Bwana, Mungu wako, atakapoongeza mpaka wako, kama alivyokuahidi, nawe utakaposema, Nataka kula nyama, kwa kuwa roho yako yatamani kula nyama; waweza kula nyama, kwa kufuata yote inayotamani roho yako. 21 Na mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako, apaweke jina lake, pakiwa mbali nawe mno, ndipo utakapochinja katika kundi lako la ng'ombe na kondoo alilokupa Bwana kama nilivyokuagiza, nawe utakula ndani ya malango yako, kwa kufuata yote inayotamani roho yako. 22 Kama vile aliwavyo paa na kulungu, ndivyo utakavyoila nyama hii; asiyekuwa tohara na aliye tohara wataila pia. 23 Ila ujihadhari kwamba usile damu, kwani ile damu ndiyo uhai; na uhai usile pamoja na nyama. 24 Usiile; imwage juu ya nchi kama maji. 25 Usiile; ili upate kufanikiwa, na watoto wako baada yako utakapofanya yaliyoelekea machoni pa Bwana. 26 Ila vitu vyako vitakatifu ulivyo navyo, na nadhiri zako, uvitwae ukaende mahali atakapochagua Bwana; 27 nawe zisongeze sadaka zako za kuteketezwa, nyama na damu, juu ya madhabahu ya Bwana, Mungu wako; na damu ya dhabihu zako uimwage juu ya madhabahu ya Bwana, Mungu wako, na wewe utakula nyama yake. 28 Maneno haya nikuagizayo yote yatunze na kuyasikiza, ili upate kufanikiwa na watoto wako baada yako milele, hapo uyafanyapo yaliyo mema na kuelekea machoni pa Bwana, Mungu wako. 29 Bwana, Mungu wako, atakapoyakatilia mbali hayo mataifa mbele yako, huko uingiako kuyamiliki, nawe ukawatwaa, na kuketi katika nchi yao; 30 ujiangalie, usije ukanaswa ukawafuata, wakiisha kuangamizwa mbele yako; wala usije ukauliza habari za miungu yao, ukisema, Mataifa haya waitumikiaje miungu yao? Nami nifanye vivyo. 31 Usimtende kama haya Bwana, Mungu wako; kwani kila yaliyo machukizo kwa Bwana, ayachukiayo yeye, wameifanyia miungu yao; kwa maana hata wana wao na binti zao huiteketezea hiyo miungu yao ndani ya moto. 32 Neno niwaagizalo lo lote liangalieni kulifanya; usiliongeze, wala usilipunguze.

Kumbukumbu la Torati 13

1 Kukizuka katikati yako nabii, au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu, 2 ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia akisema, Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo; 3 wewe usiyasikize maneno ya nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto, kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, yuawajaribu, apate kujua kwamba mwampenda Bwana, Mungu wenu, kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote. 4 Tembeeni kwa kumfuata Bwana, Mungu wenu; mcheni na kushika maagizo yake na kuisikia sauti yake, nanyi mtumikieni na kushikamana naye. 5 Na yule nabii, au yule mwotaji wa ndoto, na auawe, kwa kuwa amesema yaliyopotoka juu ya Bwana, Mungu wenu, aliyewatoa katika nchi ya Misri, akakukomboa katika nyumba ya utumwa, apate yule mtu kukupotoa katika njia aliyokuamuru Bwana, Mungu wako, uiendee. Ndivyo utakavyouondoa uovu utoke katikati yako. 6 Atakapokushawishi kwa siri ndugu yako, mwana wa mamaako, au mwana wako, au binti yako, au mke wa kifuani mwako, au rafiki yako aliye kama moyo wako, akikuambia, Twende tukaabudu miungu mingine usiyoijua wewe wala baba zako; 7 katika miungu ya mataifa yaliyo kando-kando yenu karibu nawe au mbali nawe, tokea ncha moja ya dunia hata ncha ya pili ya dunia; 8 usimkubalie wala usimsikize; wala jicho lako lisimwonee huruma, wala usimwache, wala usimfiche; 9 mwue kweli; mkono wako na uwe wa kwanza juu yake katika kumwua, na baadaye mikono ya watu wote. 10 Nawe mtupie mawe hata afe; kwa kuwa alitaka kukupotoa na Bwana, Mungu wako aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa. 11 Na Israeli wote watasikia na kuogopa, wasifanye tena uovu mfano wa huo katikati yako. 12 Ukisikia yasemwa habari ya miji yako mmojawapo, akupayo Bwana, Mungu wako, ukae humo, ukiambiwa, 13 Kumetoka katikati yako mabaradhuli kadha wa kadha, wamewapotoa wenyeji wa mji wao, wakisema, Twendeni tukaabudu miungu mingine msiyoijua; 14 ndipo nawe uulize na kutafuta, ukiuliza kwa bidii; nawe angalia, ikiwa kweli, na jambo lile halina shaka, kwamba machukizo mfano wa haya yafanyika katikati yako; 15 hakika yako uwapige wenyeji wa mji ule kwa makali ya upanga, kwa kuwaangamiza kabisa, pamoja na vitu vyote vilivyomo, na wanyama walio humo, kwa makali ya upanga. 16 Na nyara zake zote uzikusanyie katikati ya njia yake; na mji uuteketeze kwa moto, na nyara zake zote, kuwe sadaka kamili ya kuteketezwa kwa Bwana, Mungu wako; nao utakuwa magofu milele; usijengwe tena. 17 Kisishikamane na mkono wako kitu cho chote katika kitu kilichoharimishwa; ili ageuke Bwana na ukali wa hasira zake akurehemu, akuonee huruma, na kukufanya kuwa wengi, kama alivyowaapia baba zako; 18 utakaposikiza sauti ya Bwana, Mungu wako kwa kushika maagizo yake yote nikuagizayo leo, ufanye yaliyoelekea machoni pa Bwana, Mungu wako.

Kumbukumbu la Torati 14

1 Ninyi mmekuwa wana wa Bwana, Mungu wenu; msijitoje miili yenu, wala msifanye upaa katikati ya macho yenu kwa ajili ya aliyekufa. 2 Kwa kuwa u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako, na Bwana amekuchagua kuwa watu wake hasa, kuliko mataifa yote yaliyo juu ya uso wa nchi. 3 Usile kitu cho chote kichukizacho. 4 Wanyama mtakaokula ni hawa ng'ombe, na kondoo, na mbuzi, 5 kulungu, na paa, na kongoni, na mbuzi wa mwitu, na paa mweupe, na pofu, na mbuzi wa mlima; 6 na kila mnyama aliyepasuliwa ukwato, ukapasuka ukwato wake zikawa mbili, naye ni mnyama mwenye kucheua akatafuna tena, katika wanyama wote, ndiye mnyama mtakayemla. 7 Lakini, hawa msile katika wale wenye kucheua, na hao waliopasuliwa ukwato; ngamia, na sungura, na kwang'a, kwa kuwa hucheua, lakini hawakupasuliwa kwato, ni najisi kwenu; 8 na nguruwe, kwa kuwa amepasuliwa ukwato lakini hacheui, huyu ni najisi kwenu msile nyama zao, wala mizoga yao msiiguse. 9 Mtakula hawa katika wote walio majini; kila kilicho na mapezi na magamba mtakula; 10 na kila kisichokuwa na mapezi na magamba msile; ni najisi kwenu. 11 Mna ruhusa kula katika nyuni wote walio safi. 12 Lakini hawa msiwale; tai, na furukombe, na kipungu; 13 na kengewa, na kozi, na mwewe kwa aina zake; 14 na kila kunguru kwa aina zake; 15 na mbuni, na kirukanjia, na dudumizi, na kipanga kwa aina zake; 16 na bundi, na mumbi, na bundi mkubwa; 17 na mwari, na nderi, na mnandi; 18 na membe, na koikoi, kwa aina zake; na hudihudi, na popo. 19 Na wadudu wote watambaao wenye mabawa ni najisi kwenu; msiwale. 20 Mna ruhusa kula katika nyuni wote walio safi. 21 Msile nyamafu yo yote; waweza kumpa mgeni aliye ndani ya malango yako, ili apate kula; au kumliza mtu wa mataifa; kwa kuwa wewe u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako. Usimtokose mwana-mbuzi katika maziwa ya mamaye. 22 Usiache kutoa zaka ya fungu la kumi katika maongeo yote ya mbegu zako, yatokayo shamba mwaka baada ya mwaka. 23 Nawe utakula mbele za Bwana, Mungu wako, mahali atakapochagua apakalishe jina lake, zaka ya nafaka zako, na divai yako, na mafuta yako, na wazaliwa wa kwanza wa makundi yako ya ng'ombe na ya kondoo; ili upate kujifunza kumcha Bwana, Mungu wako, daima. 24 Na njia ikiwa ndefu mno nawe, usiweze kuzichukua kwa kuwa mahali ni mbali nawe mno atakapochagua Bwana, Mungu wako, apakalishe jina lake, hapo atakapokubarikia Bwana, Mungu wako; 25 ndipo uzibadili ziwe fedha, na kufunga zile fedha uende nazo mkononi mwako, hata mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako; 26 na zile fedha zitumie kwa cho chote itakachotamani roho yako, ng'ombe, au kondoo, au divai, au kileo, au roho yako itakacho kwako cho chote; nawe utakula huko mbele za Bwana, Mungu wako; tena furahi, wewe na nyumba yako; 27 na Mlawi aliye ndani ya malango yako usimwache, kwani hana fungu wala urithi pamoja nawe. 28 Kila mwaka wa tatu, mwisho wake, toa fungu la kumi lote la maongeo yako ya mwaka huo, uliweke ndani ya malango yako; 29 na Mlawi kwa kuwa hana fungu wala urithi pamoja nawe, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio ndani ya malango yako, na waje wale na kushiba; ili kwamba Bwana, Mungu wako, akubarikie katika kazi yote ya mkono wako uifanyayo.

Kumbukumbu la Torati 15

1 Kila miaka saba, mwisho wake, fanya maachilio. 2 Na jinsi ya maachilio ni hii, kila mkopeshaji na akiache alichomkopesha mwenziwe, wala asimlipize mwenziwe wala nduguye; kwa kuwa imepigwa mbiu ya maachilio ya Bwana. 3 Waweza kumtoza mgeni; lakini kila uwiacho kwa nduguyo mkono wako utamwachilia. 4 Lakini hawatakuwako maskini kwenu; (kwa kuwa Bwana atakubarikia kweli katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako, uimiliki, iwe urithi wako;) 5 kwamba utaisikiza tu kwa bidii sauti ya Bwana, Mungu wako, uyatunze maagizo haya yote nikuagizayo leo, kuyafanya. 6 Kwani Bwana, Mungu wako, atakubarikia, kama alivyokuahidi; nawe utakopesha mataifa mengi, lakini hutakopa; tena utayatawala mataifa mengi, usitawaliwe na wao. 7 Kama akiwapo mtu maskini pamoja nawe, nduguzo mmojawapo, ndani ya malango yako mojawapo, katika nchi yako akupayo Bwana, Mungu wako, usifanye moyo wako kuwa mgumu, wala usimfumbie mkono wako nduguyo maskini; 8 lakini mfumbulie mkono wako kwa kweli, umkopeshe kwa kweli yatoshayo haja yake katika ahitajiayo. 9 Jitunze, msiwe na neno lisilofaa moyoni mwako, kusema, Umekaribia mwaka wa saba, mwaka wa maachilio; jicho lako likawa ovu juu ya nduguyo usimpe kitu; naye akamlilia Bwana juu yako, ikawa ni dhambi kwako. 10 Mpe kwa kweli, wala moyo wako usisikitike utakapompa; kwa kuwa atakubarikia Bwana, Mungu wako, kwa neno hili katika kazi yako yote, na katika kila utakalotia mkono wako. 11 Kwa maana maskini hawatakoma katika nchi milele; ndipo ninakuamuru na kukuambia, Mfumbulie kwa kweli mkono wako nduguyo, mhitaji wako, maskini wako, katika nchi yako. 12 Ikiwa nduguyo, mume wa Kiebrania, au mwanamke wa Kiebrania, akiuzwa kwako, naye amekutumikia miaka sita; basi mwaka wa saba mwache huru aondoke kwako. 13 Nawe utakapomwacha huru aondoke kwako, usimwache aende zake mikono mitupu; 14 umwangalie kwa wema katika kundi lako, na sakafu yako ya nafaka, na kinu chako cha divai; mpe kama alivyokubarikia Bwana, Mungu wako. 15 Nawe kumbuka kwamba ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri, akakukomboa Bwana, Mungu wako; kwa hiyo mimi nakuamuru neno hili hivi leo. 16 Hata itakuwa, akikuambia, Siondoki kwako; kwa sababu akupenda wewe na nyumba yako, kwa kuwa yu hali njema kwako; 17 ndipo utwae uma, uupenyeze katika sikio lake uingie katika ubao wa mlango, naye atakuwa mtumishi wako milele. Na kijakazi chako naye mfanye vivyo. 18 Wala usione ugumu, utakapomwacha huru kuondoka kwako; kwani amekutumikia miaka sita kwa ujira mara mbili wa mwajiriwa; na Bwana, Mungu wako, atakubarikia kwa yote utakayofanya. 19 Wazaliwa wa kwanza waume wote wazaliwao katika kundi lako la ng'ombe na la kondoo, uwatakase kwa Bwana, Mungu wako; usifanye kazi kwa mzaliwa wa kwanza wa ng'ombe wako, wala usimkate manyoya mzaliwa wa kwanza wa kundi lako la kondoo. 20 Utamla mbele za Bwana, Mungu wako, mwaka hata mwaka mahali atakapochagua Bwana, wewe na nyumba yako. 21 Lakini akiwa na kilema, akichechea, au akiwa kipofu, au mwenye kilema kibaya cho chote, usimsongezee Bwana, Mungu wako, sadaka. 22 Utamla ndani ya malango yako; wasio tohara na wenye tohara pia watakula, kama unavyokula paa na kulungu. 23 Pamoja na haya usile damu yake; uimwage nchi kama maji.

Kumbukumbu la Torati 16

1 Utunze mwezi wa Abibu, ukamfanyie pasaka Bwana, Mungu wako, kwa kuwa ilikuwa ni mwezi wa Abibu alipokutoa Misri usiku Bwana; Mungu wako. 2 Nawe umchinjie pasaka Bwana, Mungu wako, katika kundi la kondoo na la ng'ombe, mahali atakapochagua Bwana apakalishe jina lake. 3 Usimle pamoja na mikate iliyotiwa chachu; siku saba utakula naye mikate isiyotiwa chachu, nayo ni mikate ya mateso; kwa maana ulitoka nchi ya Misri kwa haraka; ili upate kukumbuka siku uliyotoka nchi ya Misri, siku zote za maisha yako. 4 Wala isionekane kwako chachu muda wa siku saba katika mipaka yako yote; wala katika hiyo nyama uchinjayo siku ya kwanza jioni, kisilale cho chote usiku kucha hata asubuhi. 5 Usimchinje pasaka ndani ya malango yako yote akupayo Bwana, Mungu wako; 6 ila mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako, apakalishe jina lake, ndipo mtakapomchinja pasaka jioni, katika machweo ya jua, kwa wakati kama uliotoka Misri. 7 Nawe umwoke na kumla mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako; kisha asubuhi yake ugeuke uende hemani mwako. 8 Siku sita utakula mikate isiyotiwa chachu; na siku ya saba na uwe mkutano mtukufu kwa Bwana, Mungu wako, usifanye kazi yo yote. 9 Jihesabie majuma saba; tangu wakati uanzao kutia mundu katika mmea utaanza kuhesabu majuma saba. 10 Nawe sikukuu ya majuma umfanyie Bwana, Mungu wako, kwa kutoa sadaka ya hiari ya mkono wako, utakayotoa kwa kadiri akubarikiavyo Bwana, Mungu wako; 11 nawe utafurahi mbele ya Bwana, Mungu wako, wewe na mwana wako na binti yako, na mtumwa wako na mjakazi wako, na Mlawi aliye ndani ya malango yako, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio katikati yako, katika mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako, apakalishe jina lake. 12 Nawe kumbuka kwamba ulikuwa mtumwa huko Misri; tena zishike amri hizi kwa kuzifanya. 13 Fanya sikukuu ya vibanda siku saba, utakapokwisha kuyakusanya yatokayo katika sakafu yako ya nafaka, na katika kinu chako cha divai; 14 nawe utafurahi katika sikukuu yako, wewe, na mwanao, na binti yako, na mtumwa wako, na mjakazi wako, na Mlawi, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio ndani ya malango yako. 15 Siku saba mfanyie sikukuu Bwana, Mungu wako, mahali atakapochagua Bwana; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, atakubarikia katika maongeo yako yote, na katika kazi zote za mikono yako, nawe uwe katika kufurahi kabisa. 16 Mara tatu kwa mwaka na watokee wanawaume wako wote mbele za Bwana, Mungu wako, mahali atakapochagua; katika sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu, na katika sikukuu ya majuma, na katika sikukuu ya vibanda; wala wasitokee mbele za Bwana mikono mitupu. 17 Kila mtu na atoe kama awezavyo, kwa kadiri ya baraka ya Bwana, Mungu wako, alivyokupa. 18 Weka waamuzi na maakida katika malango yako yote akupayo Bwana, Mungu wako, kwa hesabu ya kabila zako; nao wawaamue watu kwa maamuzi ya haki. 19 Usipotoe maamuzi; wala usipendelee uso wa mtu; wala usitwae rushwa; kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya wenye akili, na kugeuza daawa ya wenye haki. 20 Yaliyo haki kabisa ndiyo utakayoyafuata, ili upate kuishi na kuirithi nchi upewayo na Bwana, Mungu wako. 21 Usipande mti uwao wote kuwa Ashera kwako kando ya madhabahu utakayofanya ya Bwana, Mungu wako. 22 Wala usisimamishe nguzo; ambayo Bwana, Mungu wako, aichukia.

Kumbukumbu la Torati 17

1 Usimchinjie Bwana, Mungu wako, ng'ombe wala kondoo aliye na kilema, wala neno ovu lo lote; kwa kuwa hayo ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako. 2 Ikiwa ameonekana katikati yako, ndani ya malango yako mojawapo, upewayo na Bwana, Mungu wako, mtu mume au mke afanyaye yaliyo maovu machoni pa Bwana, Mungu wako, kwa kuvunja maagano yake, 3 naye amekwenda kutumikia miungu mingine na kuiabudu, au jua, au mwezi, au vilivyo katika jeshi la mbinguni vyo vyote, nisivyoagiza mimi; 4 ukiambiwa hayo nawe umeyasikia, ndipo utafute kwa bidii, na tazama, ikiwa ni kweli lina hakika jambo lile, kuwa yafanywa machukizo kama hayo katika Israeli; 5 ndipo umchukue nje malangoni kwako, yule mtu mume, au yule mwanamke, aliyefanya jambo lile ovu; ukawapige kwa mawe, wafe. 6 Huyo atakayeuawa na auawe kwa midomo ya mashahidi wawili, au mashahidi watatu; asiuawe kwa mdomo wa shahidi mmoja. 7 Mikono ya wale mashahidi na iwe juu yake kwanza kwa kumwua, kisha mikono ya watu wote. Uondoe vivyo uovu katikati yako. 8 Ikiwa limezuka neno lililo zito kukupita wewe, katika maamuzi kati ya damu na damu, na kati ya daawa na daawa, na kati ya pigo na pigo, nayo yashindaniwa katika malango yako; ndipo nawe uondoke, ukwee uende mahali atakapochagua Bwana, Mungu wako; 9 uwaendee makuhani Walawi, na mwamuzi atakayekuwako siku hizo; uwaulize; nao watakuonyesha hukumu ya maamuzi; 10 nawe fanya sawasawa na hukumu watakayokuonyesha mahali hapo atakapochagua Bwana; nawe tunza kufanya kwa mfano wa yote watakayokufunza; 11 kwa mfano wa sheria watakayokufunza, na kwa mfano wa hukumu watakayokuambia, fanya vivyo; usigeuke katika hukumu watakayokuonyesha, kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto. 12 Na mtu afanyaye kwa kujikinai, kwa kutomsikiza kuhani asimamaye hapo kwa kumtumikia Bwana, Mungu wako, au mwamuzi, na afe mtu huyo; nawe utauondoa uovu katika Israeli. 13 Na hao watu wote watasikia na kuogopa, wasifanye tena kwa kujikinai. 14 Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako ukaimiliki, na kukaa humo; nawe utakaposema, Nitaweka mfalme juu yangu mfano wa mataifa yote yaliyo kando-kando yangu; 15 usiache kumweka yule atakayechaguliwa na Bwana, Mungu wako, awe mfalme juu yako; umweke mmoja katika ndugu zako awe mfalme juu yako; usimtawaze mgeni juu yako, ambaye si ndugu yako. 16 Ila asifanye farasi wake kuwa wengi, wala asiwarudishe watu Misri, ili apate kufanya farasi kuwa wengi; kwa kuwa Bwana amewaambia, Tangu sasa msirudie tena njia ile. 17 Wala asijizidishie wake, ili moyo wake usikengeuke; wala asifanye fedha zake na dhahabu kuwa nyingi mno. 18 Tena na iwe, zamani aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, kufuata hicho kilicho mbele ya makuhani Walawi; 19 na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha Bwana, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya; 20 moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake, wala asikengeuke katika maagizo, kwa mkono wa kuume wala wa kushoto; ili apate kuzifanya siku zake kuwa nyingi katika ufalme wake, yeye na wanawe, katikati ya Israeli.

Kumbukumbu la Torati 18

1 Makuhani Walawi, kabila yote ya Lawi, wasiwe na fungu wala urithi pamoja na Israeli; watakula sadaka za Bwana zifanywazo kwa moto, na urithi wake. 2 Wala wasiwe na urithi kati ya ndugu zao; Bwana ndiye urithi wao, kama alivyowaambia. 3 Na hii itakuwa haki ya makuhani kwa watu hao wasongezao sadaka, ikiwa ni ng'ombe au kondoo wampe kuhani mkono, na mashavu mawili, na tumbo. 4 Malimbuko ya nafaka zako, na divai yako, na mafuta yako, na manyoya ya kwanza ya kondoo zako, umpe. 5 Kwani Bwana, Mungu wako, amemchagua katika kabila zako zote, asimame atumike kwa jina la Bwana, yeye na wanawe milele. 6 Na akija Mlawi atokaye katika malango yako mojawapo, katika Israeli yote alipokuwa akikaa, akaja kwa mapenzi yote ya nafsi yake mahali atakapochagua Bwana; 7 na atumike kwa jina la Bwana, Mungu wake, kama wafanyavyo ndugu zake wote, Walawi wasimamao huko mbele za Bwana. 8 Wawe na fungu sawasawa la kula, pamoja na haya yaliyomfikilia kwa kuuzwa urithi wa baba zake. 9 Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale. 10 Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, 11 wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. 12 Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa Bwana; kisha ni kwa sababu ya hayo Bwana, Mungu wako, anawafukuza mbele yako. 13 Uwe mkamilifu kwa Bwana, Mungu wako. 14 Maana mataifa haya utakaowamiliki huwasikiliza wanaoshika nyakati mbaya na kutazama bao; bali wewe, Bwana, Mungu wako, hakukupa ruhusa kutenda hayo. 15 Bwana, Mungu wako, atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zako kama nilivyo mimi; msikilizeni yeye. 16 Kama vile ulivyotaka kwa Bwana, Mungu wako, huko Horebu, siku ya kusanyiko, ukisema, Nisisikie tena sauti ya Bwana, Mungu wangu, wala nisiuone tena moto huu mkubwa, nisije nikafa. 17 Bwana akaniambia, Wametenda vema kusema walivyosema. 18 Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru. 19 Hata itakuwa, mtu asiyesikiliza maneno yangu atakayosema yule kwa jina langu, nitalitaka kwake. 20 Lakini nabii atakayenena neno kwa kujikinai kwa jina langu, ambalo sikumwagiza kulinena, au atakayenena katika jina la miungu mingine, nabii yule atakufa. 21 Nawe ukisema moyoni mwako, Tutajuaje neno asilolinena Bwana? 22 Atakaponena nabii kwa jina la Bwana, lisifuate jambo lile wala kutimia, hilo ndilo neno asilolinena Bwana; kwa kujikinai amelinena huyo nabii, usimwogope

Kumbukumbu la Torati 19

1 Bwana, Mungu wako, atakapoyakatilia mbali hayo mataifa yenye nchi akupayo Bwana, Mungu wako, nawe ukawafuata, na kukaa katika miji yao, na katika nyumba zao; 2 itenge miji mitatu iwe kwako katikati ya nchi yako, akupayo Bwana, Mungu wako, kuimiliki. 3 Itengeze njia, igawanye na mipaka ya nchi yako, akurithishayo Bwana, Mungu wako, iwe mafungu matatu, ili kwamba kila mwenye kuua mtu apate kukimbilia huko. 4 Na hii ndiyo hukumu ya mwenye kuua mtu, atakayekimbilia huko awe hai; atakayemwua mwenziwe pasipo kukusudia, wala hakumchukia tangu hapo; 5 kama aingiapo mtu na mwenziwe mwituni kwenda kukata kuni, akapeleka mkono wake na shoka ili kukata mti, likatoka shoka katika mpini, likampiga yule mwenziwe hata akafa; basi na akimbilie katika miji hii mmojawapo awe hai; 6 asije akaandamiwa mwuaji na mwenye kulipiza kisasi cha damu, moyo wake ukali na hasira, akampata kwa njia kuwa ndefu, akamwua; wala hana haki ya kuuawa, kwa kuwa hakumchukia tangu hapo. 7 Kwa sababu hii ninakuamuru, na kukuambia, Ujitengee miji mitatu. 8 Na kama Bwana, Mungu wako, akiueneza mpaka wako kama alivyowaapia baba zako, akakupa na nchi yote aliyoahidi kwamba atawapa baba zako; 9 nawe ukiyashika maagizo haya yote nikuagizayo leo, na kuyafanya, kumpenda Bwana, Mungu wako, na kwenda sikuzote katika njia zake, ndipo ujiongezee miji mitatu tena, pamoja na mitatu ile; 10 isije ikamwagika damu ya asiye makosa kati ya nchi yako akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi, ikawa na damu juu yako. 11 Lakini mtu awaye yote akimchukia mwenziwe na kumwotea na kumwinukia, akampiga hata akafa; naye akakimbilia miji hii mmojawapo; 12 ndipo wazee wa mji wake wapeleke ujumbe kumtwaa huko, na kumuua katika mkono wa mwenye kulipiza kisasi cha damu, apate kufa. 13 Jicho lako lisimhurumie, lakini uondoe damu ya asiye makosa katika Israeli, ili upate kufanikiwa. 14 Usiiondoe alama ya mpaka wa jirani yako, waliouweka watu wa kale katika urithi wako, utakaorithi ndani ya nchi akupayo Bwana, Mungu wako, uimiliki. 15 Shahidi mmoja asimwinukie mtu awaye yote kumshuhudia kwa uovu wo wote, wala kwa dhambi yo yote, katika makosa akosayo yo yote; jambo na lithibitishwe kwa vinywa vya mashahidi wawili, au watatu. 16 Shahidi mdhalimu akimwinukia mtu ye yote na kushuhudia juu yake ya upotoe; 17 ndipo wale watu washindanao kwa mambo yale na wasimame wote wawili mbele za Bwana, mbele ya makuhani na waamuzi watakaokuwapo siku hizo; 18 nao waamuzi na watafute kwa bidii; na tazama, yule shahidi akiwa shahidi wa uongo, naye ametoa ushahidi wa uongo juu ya nduguye; 19 ndipo mtamfanyia kama alivyodhani kumfanyia nduguye; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako. 20 Na watakaosalia watasikia na kuogopa, wasifanye tena uovu mfano wa huo katikati yako. 21 Wala jicho lako lisiwe na huruma; uzima kwa uzima, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu.

Kumbukumbu la Torati 20

1 Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe, usiwaogope; kwa kuwa Bwana Mungu wako, yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi ya Misri. 2 Na iwe, msongeapo mapiganoni, kuhani na akaribie na kusema na watu, 3 awaambie, Sikizeni, enyi Israeli, hivi leo mwasongea mapiganoni juu ya adui zenu mioyo yenu na isizime; msiche, wala msiteteme, wala msiingiwe na hofu kwa ajili ya wao; 4 kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye awaandamaye kwenda kuwapigania juu ya adui zenu, ili kuwaokoa ninyi. 5 Na maakida na waseme na watu, na kuwaambia, Ni mtu gani aliye hapa aliyejenga nyumba mpya, wala hajaiweka wakfu? Aende akarudi nyumbani kwake, asije akafa mapiganoni, ikawekwa wakfu na mtu mwingine. 6 Ni mtu gani aliye hapa aliyepanda shamba la mizabibu, wala hajatumia matunda yake? Aende akarudi nyumbani kwake asije akafa mapiganoni, yakatumiwa na mtu mwingine matunda yake. 7 Ni mtu gani aliye hapa aliyemposa mke wala hajaoa? Aende akarudi nyumbani kwake asije akafa mapiganoni, huyo mwanamke akaolewa na mume mwingine. 8 Tena maakida na waseme zaidi na watu, wawaambie, Ni mtu gani aliye hapa tena mwenye hofu na moyo mnyonge? Aende akarudi nyumbani kwake, isije mioyo ya nduguze ikayeyuka mfano wa moyo wake. 9 Itakuwa hapo watakapokwisha wale maakida kusema na watu, na waweke majemadari wa majeshi juu ya watu. 10 Utakaposongea karibu ya mji kwenda kupigana juu yake, ndipo utakapowapigia ukelele wa amani. 11 Itakuwa utakapokujibu kwa amani, na kukufungulia, ndipo watu wote watakaoonekana humo watakufanyia kazi ya shokoa, na kukutumikia. 12 Na kwamba hautaki kufanya amani nawe, lakini utafanya vita juu yako, ndipo uuhusuru; 13 na Bwana, Mungu wako, autiapo mkononi mwako, mpige kila mume aliyemo kwa makali ya upanga; 14 lakini wanawake na watoto, na wanyama wa miji, na vilivyo mjini vyote, navyo ni nyara zake zote, uvitwae viwe mateka kwako; nawe utakula nyara za adui zako alizokupa Bwana, Mungu wako. 15 Utaifanyia vivyo miji yote iliyo mbali sana nawe, isiyokuwa miji ya mataifa haya. 16 Lakini katika miji ya mataifa haya akupayo Bwana, Mungu wako, kuwa urithi, usihifadhi kuwa hai kitu cho chote kipumzikacho; 17 lakini uwaangamize kabisa, Mhiti, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, kama alivyokuamuru Bwana, Mungu wako; 18 wasije wakawafunza kufanya mfano wa machukizo yao yote, waliyoifanyia miungu yao; hivyo itakuwa ni makosa juu ya Bwana, Mungu wenu. 19 Wewe utakapohusuru mji siku nyingi kwa kufanya vita juu yake, upate kuutwaa, usiangamize miti yake kwa kupeleka shoka juu yake, kwani utaweza kula matunda yake; wala usiiteme, kwa maana huo mti wa kondeni, je! Ni mtu, hata ukauzuie? 20 Ila miti uijuayo si miti ya kuliwa iangamize, na kuitema; ukajenge maburuji juu ya mji ufanyao vita juu yako, hata uanguke.

Kumbukumbu la Torati 21

1 Aonekanapo mtu ameuawa katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako, kuimiliki, amelala kondeni, wala haijulikani ni nani aliyempiga; 2 na watoke nje wazee wako na waamuzi wako, nao wapime hapo mpaka miji iliyomzunguka huyo aliyeuawa; 3 na iwe, mji ulio karibu na yule aliyeuawa, wale wazee wake mji huo watwae mtamba katika kundi la ng'ombe, ambaye hajafanya kazi, wala hajakokota jembe la nira; 4 wazee wa mji huo na wamshushe yule mtamba mpaka bonde lenye maji ya mtoni, lisilolimwa wala kupandwa, wakamvunje yule mtamba shingo yake humo bondeni; 5 nao makuhani wana wa Lawi wasongee karibu, kwa kuwa ndio aliowachagua Bwana, Mungu wako, wamtumikie, na kubariki katika jina la Bwana na kila neno lishindaniwalo, na kila pigo, litakuwa kwa kufuata maneno yao; 6 na wazee wote wa mji ule, ulio karibu sana na yule aliyeuawa, na waoshe mikono yao juu ya huyo mtamba aliyevunjwa shingo yake humo bondeni; 7 na wajibizane kwamba, Mikono yetu haikumwaga damu hii, wala macho yetu hayakuiona. 8 Ee Bwana, samehe watu wako Israeli, uliowakomboa, wala usiache damu ya asiye makosa ikakaa katikati ya watu wako Israeli. Na ile damu utasamehewa kwao. 9 Ndivyo utakavyoondoa damu ya asiye makosa katikati yako, utakapofanya yaliyo sawa machoni pa Bwana. 10 Utakapokwenda vitani kupigana juu ya adui zako, na Bwana, Mungu wako, awatiapo mikononi mwako, nawe uwachukuapo mateka, 11 ukaona kati ya mateka mwanamke mzuri, ukafanya tamaa kwake, ukawaza kumtwaa kuwa mkeo; 12 ndipo umchukue kwenu nyumbani kwako, naye atanyoa kichwa, akate na kucha; 13 avue na mavazi ya uteka wake akae nyumbani mwako, awakalie matanga babaye na mamaye mwezi mzima, kisha uingie kwake uwe mumewe, naye awe mkeo. 14 Tena utakapokuwa huna furaha naye, mpe ruhusa aende atakako; lakini usimwuze kabisa kwa fedha, usimfanye kama mtumwa, kwa kuwa ulimtweza. 15 Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa; 16 ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu; 17 lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye. 18 Mtu akiwa na mwana mkaidi, mshupavu, asiyetii sauti ya baba yake, wala sauti ya mama yake, nao wajapomwadhibu hawasikizi, 19 ndipo babaye na mamaye na wamkamate, na kumpeleka kwa wazee wa mji wake, katika lango la mahali pake; 20 wawaambie wazee wa mji wake, Huyu mwana wetu ni mkaidi, mshupavu, hasikizi sauti yetu; ni mwasherati, tena ni mlevi. 21 Waume wote wa mji wake na wamtupie mawe, afe; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako; na Israeli wote watasikia na kuogopa. 22 Akiwa mtu ametenda dhambi ipasayo kufa, akauawa, nawe ukamtundika juu ya mti; 23 mzoga wake usikae usiku kucha juu ya mti; lazima utamzika siku iyo hiyo; kwani aliyetundikwa amelaaniwa na Mungu; usije ukatia unajisi katika nchi yako akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi wako.

Kumbukumbu la Torati 22

1 Umwonapo ng'ombe wa nduguyo au kondoo wake akipotea, usijifiche kama usiyemwona; sharti utamrudisha kwa nduguyo. 2 Na kwamba yule nduguyo hayupo karibu nawe, au ukiwa humjui, umchukue kwenu nyumbani kwako, uwe naye hata aje nduguyo kumtafuta, nawe mrudishie. 3 Tena fanya vivyo kwa punda wake; tena fanya vivyo kwa mavazi yake; tena fanya vivyo kwa kila kitu kilichopotea cha nduguyo, kilichompotea ukakiona wewe; usijifiche kama usiyekiona. 4 Umwonapo punda wa nduguyo, au ng'ombe wake, ameanguka kando ya njia, usijifiche kama usiyemwona; sharti umsaidie kumwinua tena. 5 Mwanamke asivae mavazi yampasayo mwanamume, wala mwanamume asivae mavazi ya mwanamke; kwa maana kila afanyaye mambo hayo ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako. 6 Kiota cha ndege kikitukia kuwa mbele yako njiani, katika mti wo wote, au chini, chenye makinda au mayai, naye koo ameatamia juu ya makinda, au juu ya mayai, usimtwae yule koo pamoja na makinda; 7 sharti umwache yule koo aende zake, lakini makinda waweza kuyatwaa uwe nayo; ili upate kufanikiwa, ufanye siku zako kuwa nyingi. 8 Utakapojenga nyumba mpya, fanya ukuta kando-kando ya dari lako, usije ukaleta damu juu ya nyumba yako, mtu akianguka huko. 9 Usipande shamba lako la mizabibu aina mbili za mbegu; yasije yakaondolewa matunda yote, mbegu ulizopanda na maongeo ya mizabibu yako. 10 Usilime kwa ng'ombe na punda wakikokota jembe pamoja. 11 Usivae nguo iliyochanganyikana sufu na kitani pamoja. 12 Ujifanyizie vishada katika pembe nne za mavazi yako ya kujifunika. 13 Mtu akitwaa mke, akamwingilia na kumchukia, 14 kisha akamshitaki mambo ya aibu kumzushia jina baya, akasema, Nimemtwaa mwanamke huyu, nami nilipomkaribia sikuona kwake alama za ubikira; 15 ndipo babaye yule kijana na mamaye watakapotwaa alama za yule kijana za ubikira, wawatolee wazee wa mji langoni; 16 na baba yake yule kijana awaambie wazee, Mwanamume huyu nilimpa binti yangu awe mkewe, naye amchukia; 17 angalieni, amemwekea mambo ya aibu, asema, Sikuona kwa binti yako alama za ubikira, nazo hizi ndizo alama za binti yangu za ubikira. Na wayakunjue yale mavazi mbele ya wazee wa mji. 18 Basi wazee wa mji ule na wamtwae yule mtu mume na kumrudi, 19 wamtoze shekeli mia za fedha, wampe babaye yule kijana, kwa kuwa amemzulia jina baya mwanamwali wa Israeli; naye awe mkewe; hana ruhusa ya kumwacha siku zake zote. 20 Lakini likiwa ni kweli neno hili, la kutoonekana kwake yule kijana alama za ubikira; 21 na wamtoe nje yule kijana mlangoni pa nyumba ya baba yake, na waume wa mji wake wampige kwa mawe hata afe; kwa vile alivyofanya upumbavu katika Israeli, kwa kufanya ukahaba katika nyumba ya baba yake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako. 22 Akifumaniwa mtu mume amelala na mwanamke aliyeolewa na mume, na wafe wote wawili, mtu mume aliyelala na mwanamke, na yule mwanamke naye; ndivyo utakavyoondoa uovu katika Israeli. 23 Pakiwa na kijana aliye mwanamwali ameposwa na mume, na mwanamume akimkuta mjini, akalala naye; 24 watoeni nje katika lango la mji ule, mkawapige kwa mawe hata wafe; yule kijana, kwa kuwa hakupiga ukelele, naye yu ndani ya mji; na yule mume, kwa kuwa amemtweza mke wa mwenzake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako. 25 Lakini yule mtu mume kama akimkuta kondeni kijana aliyeposwa, naye mume akamtenza nguvu, akalala naye; yule mtu mume aliyelala naye na afe pekee; 26 lakini yule kijana usimfanye neno; hana dhambi yule kijana ipasayo kuuawa, kwa kuwa ni mfano wa mtu kumwondokea mwenzake akamwua, ni vivyo lilivyo jambo hili; 27 kwani alimkuta kondeni; yule kijana aliyeposwa akalia, pasiwe na mtu wa kumwokoa. 28 Mtu mume akimwona kijana aliye mwanamwali ambaye hajaposwa, akamshika na kulala naye, wakaonekana; 29 yule mtu mume aliyelala naye na ampe baba yake yule kijana shekeli hamsini za fedha, kisha na awe mkewe, kwa kuwa amemtweza; hana ruhusa ya kumwacha siku zake zote. 30 Mtu mume asimtwae mke wa baba yake, wala asifunue ncha ya mavazi ya baba yake.

Kumbukumbu la Torati 23

1 Aliyejeruhika konde, au aliyekatika tupu yake, asiingie mtu huyo katika mkutano wa Bwana. 2 Mwana wa haramu asiingie katika mkutano wa Bwana; hata kizazi cha kumi asiingie aliye wake katika mkutano wa Bwana. 3 Mwamoni wala Mmoabi wasiingie katika mkutano wa Bwana; wala hata kizazi cha kumi mtu wao asiingie katika mkutano wa Bwana milele; 4 kwa sababu hapo mlipotoka Misri hawakuwalaki na chakula wala maji njiani; na kwa kuwa walimwajiri juu yako Balaamu mwana wa Beori kutoka Pethori iliyo Mesopotamia, aje akuapize. 5 Lakini Bwana, Mungu wako, hakukubali kumsikiza huyo Balaamu; Bwana, Mungu wako, aliyageuza yale maapizo kuwa ni baraka, kwa vile alivyokupenda Bwana, Mungu wako. 6 Usitafute amani yao wala heri yao siku zako zote, milele. 7 Usimchukie Mwedomi; kwa kuwa ni ndugu yako; usimchukie Mmisri, kwa kuwa ulikuwa mgeni katika nchi yake. 8 Wana wao watakaozaliwa kizazi cha tatu na waingie katika mkutano wa Bwana. 9 Utakapotoka kwenda juu ya adui zako nawe u katika marago, jilinde na kila neno baya. 10 Akiwa kwenu mtu awaye yote asiyekuwa ni tohara kwa ajili ya yaliyomtukia usiku, na atoke nje ya kituo, wala asiingie ndani ya kituo; 11 lakini na iwe ikaribiapo jioni, yeye ataoga maji; na jua likiisha kuchwa ataingia ndani ya kituo. 12 Tena uwe na mahali nje ya kituo, kwa kutokea nje; 13nawe uwe na jembe dogo katika silaha zako; napo uotamapo nje uchimbe kwa lile jembe, na kugeuka na kukifunika kikutokacho; 14 kwa kuwa Bwana. Mungu wako, yuatembea katika kituo akuokoe, na kukutolea adui zako mbele yako; kwa hiyo na kiwe kitakatifu kituo chako; asije akaona kitu kwako kisichokuwa safi, akageuka na kukuacha. 15 Usimrudishe kwa bwana wake mtumwa aliyejiponya kutoka kwa bwana wake kuja kwako; 16na akae nawe, katikati yako, ndani ya malango yako mojawapo, mahali atakapochagua palipo pema machoni pake; usimwonee. 17 Pasiwe na kahaba katika binti za Israeli, wala pasiwe na hanithi katika wana wa Israeli wanaume. 18 Usilete ujira wa kahaba, wala mshahara wa mbwa, katika nyumba ya Bwana, Mungu wako, kwa ajili ya nadhiri yo yote; kwani haya ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako, yote mawili. 19 Usimkopeshe ndugu yako kwa riba; riba ya fedha, riba ya vyakula, riba ya kitu cho chote kikopeshwacho kwa riba; 20 mgeni waweza kumkopesha kwa riba, ila usimkopeshe ndugu yako kwa riba; ili Bwana, Mungu wako, apate kukubarikia katika yote utiayo mkono wako, katika nchi uingiayo kuimiliki. 21 Utakapoweka nadhiri kwa Bwana, Mungu wako, usiwe mlegevu katika kuiondoa; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, hataacha kuitaka kwako; nayo hivi itakuwa dhambi kwako. 22 Lakini ukijizuia usiweke nadhiri, haitakuwa dhambi kwako. 23 Yaliyotoka midomoni mwako yashike kuyafanya; kwa mfano wa ulivyomwekea nadhiri Bwana, Mungu wako, ni sadaka ya hiari uliyoahidi kwa kinywa chako. 24 Uingiapo katika shamba la mizabibu la jirani yako, utaweza kula zabibu za kukushibisha, kama upendavyo; ila usitie katika chombo chako. 25 Uingiapo katika mmea wa jirani yako waweza kuyapurura masuke kwa mkono wako; ila usisongeze mundu katika mmea wa jirani yako.

Kumbukumbu la Torati 24

1 Mtu akiisha kutwaa mke kwa kumwoa, asipopata kibali machoni mwake, kwa kuwa ameona neno ovu kwake, na amwandikie hati ya kumwacha, akamtilie mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake. 2 Naye akiisha kuondoka katika nyumba yake, ana ruhusa kwenda akawa mke wa mtu mwingine. 3 Na huyo mumewe wa sasa akimchukia, na kumwandikia hati ya kumwacha, na kumpa mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake; au akifa yeye mumewe wa sasa, aliyemtwaa kuwa mkewe; 4 yule wa kwanza aliyemwacha asimtwae kuwa mkewe tena, akiisha kutiwa unajisi; kwa kuwa haya ni machukizo mbele za Bwana; kwa hiyo usiitie dhambini nchi, akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi. 5 Mtu atwaapo mke mpya, asiende vitani pamoja na jeshi, wala asipewe shughuli juu yake yo yote; akae faragha mwaka mmoja nyumbani mwake, apate mfurahisha mkewe aliyemtwaa. 6 Mtu awaye yote asitwae jiwe la kusagia, la juu wala la chini, kuwa rehani; kwani hivi ni kutwaa maisha ya mtu kuwa rehani. 7 Mtu akionekana anamwiba nduguze mmojawapo katika wana wa Israeli, akamfanya kama mtumwa, au kumwuza; na afe mwivi huyo; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako. 8 Angalia katika pigo la ukoma, utunze kwa bidii, kwa kufanya mfano wa yote watakayowafundisha makuhani Walawi; tunzeni kwa kuyafanya vile vile kama nilivyowaamuru wao. 9 Kumbukeni na Bwana, Mungu wako alivyomtenda Miriamu katika njia mlipotoka Misri. 10 Umkopeshapo jirani yako cho chote kikopeshwacho usiingie katika nyumba yake kwenda kutwaa rehani kwake. 11 Simama nje, yule umkopeshaye akuletee nje ile rehani. 12 Naye akiwa ni mtu maskini, usilale na rehani yake. 13 Sharti umrudishie rehani lichwapo jua, apate kulala na mavazi yake, na kukubarikia; nayo itakuwa ni haki kwako mbele za Bwana, Mungu wako. 14Usimwonee mtumishi mwenye ujira aliye maskini na uhitaji, kama ni wa nduguzo, au kama ni wageni wako mmojawapo walio katika nchi yako, ndani ya malango yako; 15 mpe ujira wake kwa siku yake, wala jua lisichwe juu yake; kwa maana ni maskini, moyo wake umeutumainia huo; asije akamlilia Bwana juu yako, ikawa ni dhambi kwako. 16 Mababa wasiuawe kwa ajili ya watoto wao, wala watoto wasiuawe kwa ajili ya baba zao; kila mtu na auawe kwa ajili ya dhambi yake mwenyewe. 17 Usipotoshe hukumu ya mgeni, wala ya yatima; wala usitwae mavazi ya mjane, yawe rehani; 18 bali kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika Misri, Bwana, Mungu wako, akakukomboa huko; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili. 19 Uvunapo mavuno yako katika shamba lako, ukasahau mganda shambani, usirudi kuuchukua; na uwe wa mgeni, au yatima, au mjane; ili Bwana, Mungu wako, akubariki katika kazi yote ya mikono yako. 20 Utakapochuma matunda ya mizeituni yako, usirudi kuchuma mara ya pili; yaliyobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane. 21 Uchumapo zabibu katika shamba lako la mizabibu, usichume mara ya pili; zilizobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane. 22 Nawe kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili.

Kumbukumbu la Torati 25

1 Pakiwa na mashindano kati ya watu, wakaenda maamuzini, na hao waamuzi wakawaamua; na wampe haki mwenye haki, na wamhukumie makosa yule mwovu; 2 na iwe, ikimpasa kupigwa yule mwovu, alazwe chini na mwamuzi, na kupigwa mbele ya uso wake, kwa kadiri ya uovu wake, kwa kuhesabu. 3 Aweza kumpiga fimbo arobaini asizidishe asije akaonekana nduguyo kuwa amedharauliwa kwako, azidishapo kwa kumpiga fimbo nyingi juu ya hizi. 4 Ng'ombe apurapo nafaka usimfunge kinywa. 5 Watakapoketi pamoja mtu na nduguye, mmojawapo akafa, wala hana mwana wa kiume, mke wa yule aliyekufa asiolewe nje na mgeni; nduguye yule mumewe amwingilie amweke kwake awe mkewe, kumfanyia yampasayo nduguye mumewe. 6 Na iwe, yule mzaliwa wa kwanza atakayemzaa, amfuate nduguye aliyekufa kwa jina lake, lisije likafutwa jina lake katika Israeli. 7 Na yule mtu kwamba hapendi kumtwaa mke wa nduguye, aende huyo mke wa nduguye langoni kwa wazee, akawaambie, Nduguye mume wangu yuakataa kumsimamishia nduguye jina katika Israeli, hataki kunitimizia yampasayo nduguye mume wangu. 8 Ndipo wamwite wazee wa mji wake waseme naye; naye akisimama na kusema, Sitaki mimi kumtwaa mwanamke huyu, 9 ndipo mke wa nduguye amkaribie mbele ya hao wazee, amvue kiatu chake mguuni mwake, na kumtemea mate ya uso; kisha atajibu yule mwanamke, aseme, Mume akataaye kumjengea nduguye nyumba yake na afanywe hivi. 10 Na jina lake katika Israeli liitwe, Nyumba ya mvuliwa kiatu. 11 Washindanapo waume wao kwa wao, akakaribia mke wa mmojawapo, ili kumwokoa mumewe katika mkono wa ampigaye, yule mke akatoa mkono wake, na kumkamata tupu yake; 12 umkate ule mkono wake, lisiwe na huruma jicho lako. 13 Usiwe na mawe ya kupimia mbalimbali, kubwa na dogo, katika mfuko wako. 14 Usiwe na vipimo mbalimbali, kikubwa na kidogo, katika nyumba yako. 15 Uwe na jiwe timilifu la haki, uwe na kipimo kitimilifu cha haki; zipate kuwa nyingi siku zako, katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako. 16 Kwa kuwa wote wayatendao mambo kama haya, wote watendao yasiyo haki, ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako. 17 Kumbuka aliyokufanya Amaleki katika njia mlipokuwa mkitoka Misri; 18 jinsi alivyokukuta katika njia, akapiga katika watu wako walioachwa nyuma, wote waliokuwa wanyonge nyuma yako, ulipokuwa umechoka na kuzimia; wala asimche Mungu. 19 Basi itakuwa, hapo atakapokwisha kukupumzisha Bwana, Mungu wako, katika adui zako wote walio kando-kando, katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi uimiliki, ndipo uufute ukumbuko wa Amaleki chini ya mbingu; usisahau.

Kumbukumbu la Torati 26

1 Pakiwa na mashindano kati ya watu, wakaenda maamuzini, na hao waamuzi wakawaamua; na wampe haki mwenye haki, na wamhukumie makosa yule mwovu; 2 na iwe, ikimpasa kupigwa yule mwovu, alazwe chini na mwamuzi, na kupigwa mbele ya uso wake, kwa kadiri ya uovu wake, kwa kuhesabu. 3 Aweza kumpiga fimbo arobaini asizidishe asije akaonekana nduguyo kuwa amedharauliwa kwako, azidishapo kwa kumpiga fimbo nyingi juu ya hizi. 4 Ng'ombe apurapo nafaka usimfunge kinywa. 5 Watakapoketi pamoja mtu na nduguye, mmojawapo akafa, wala hana mwana wa kiume, mke wa yule aliyekufa asiolewe nje na mgeni; nduguye yule mumewe amwingilie amweke kwake awe mkewe, kumfanyia yampasayo nduguye mumewe. 6 Na iwe, yule mzaliwa wa kwanza atakayemzaa, amfuate nduguye aliyekufa kwa jina lake, lisije likafutwa jina lake katika Israeli. 7 Na yule mtu kwamba hapendi kumtwaa mke wa nduguye, aende huyo mke wa nduguye langoni kwa wazee, akawaambie, Nduguye mume wangu yuakataa kumsimamishia nduguye jina katika Israeli, hataki kunitimizia yampasayo nduguye mume wangu. 8 Ndipo wamwite wazee wa mji wake waseme naye; naye akisimama na kusema, Sitaki mimi kumtwaa mwanamke huyu, 9 ndipo mke wa nduguye amkaribie mbele ya hao wazee, amvue kiatu chake mguuni mwake, na kumtemea mate ya uso; kisha atajibu yule mwanamke, aseme, Mume akataaye kumjengea nduguye nyumba yake na afanywe hivi. 10 Na jina lake katika Israeli liitwe, Nyumba ya mvuliwa kiatu. 11 Washindanapo waume wao kwa wao, akakaribia mke wa mmojawapo, ili kumwokoa mumewe katika mkono wa ampigaye, yule mke akatoa mkono wake, na kumkamata tupu yake; 12 umkate ule mkono wake, lisiwe na huruma jicho lako. 13 Usiwe na mawe ya kupimia mbalimbali, kubwa na dogo, katika mfuko wako. 14 Usiwe na vipimo mbalimbali, kikubwa na kidogo, katika nyumba yako. 15 Uwe na jiwe timilifu la haki, uwe na kipimo kitimilifu cha haki; zipate kuwa nyingi siku zako, katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako. 16 Kwa kuwa wote wayatendao mambo kama haya, wote watendao yasiyo haki, ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako. 17 Kumbuka aliyokufanya Amaleki katika njia mlipokuwa mkitoka Misri; 18 jinsi alivyokukuta katika njia, akapiga katika watu wako walioachwa nyuma, wote waliokuwa wanyonge nyuma yako, ulipokuwa umechoka na kuzimia; wala asimche Mungu. 19 Basi itakuwa, hapo atakapokwisha kukupumzisha Bwana, Mungu wako, katika adui zako wote walio kando-kando, katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi uimiliki, ndipo uufute ukumbuko wa Amaleki chini ya mbingu; usisahau.

Kumbukumbu la Torati 27

1 Musa na wazee wa Israeli wakawaagiza wale watu wakawaambia, Shikeni maagizo yote niwaagizayo leo. 2 Na iwe, siku mtakayovuka Yordani kwenda nchi akupayo Bwana, Mungu wako, ujisimamishie mawe makubwa, ukayatalize matalizo, 3 uyaandike maneno yote ya torati hii juu yake, utakapokwisha kuvuka; ili upate kuingia nchi akupayo Bwana, Mungu wako, nchi imiminikayo maziwa na asali, kama alivyokuahidi Bwana, Mungu wa baba zako. 4 Na iwe, mtakapokwisha vuka Yordani myasimamishe mawe haya, niwaagizayo hivi leo, katika mlima Ebali, nawe yatalize matalizo. 5 Na huko umjengee madhabahu Bwana, Mungu wako, madhabahu ya mawe, usitumie chombo cha chuma juu yake. 6 Jenga hiyo madhabahu ya Bwana, Mungu wako, kwa mawe yasiyochongwa; ukamtolee Bwana, Mungu wako, sadaka za kuteketezwa juu yake; 7 ufanye na sadaka za amani, ukale huko; nawe furahi mbele za Bwana, Mungu wako. 8 Kisha, andika juu ya mawe hayo maneno ya torati hii yote, waziwazi sana. 9 Musa na makuhani Walawi wakawaambia Israeli wote wakasema, Nyamaza, usikize, Ee Israeli; leo umekuwa watu wa Bwana, Mungu wako. 10 Basi isikize sauti ya Bwana, Mungu wako, ufanye maagizo yake na amri zake nikuagizavyo leo. 11 Musa akawaagiza wale watu siku iyo hiyo, akasema, 12 Hawa na wasimame juu ya mlima wa Gerizimu kwa kuwabarikia watu, mkiisha vuka Yordani; Simeoni, na Lawi, na Yuda, na Isakari, na Yusufu, na Benyamini; 13 na hawa na wasimame juu ya mlima wa Ebali kwa laana; Reubeni, na Gadi, na Asheri, na Zabuloni, na Dani, na Naftali. 14 Kisha Walawi na wajibu, wawaambie watu wote wa Israeli kwa sauti kuu, 15 Na alaaniwe mtu afanyaye sanamu ya kuchonga, au ya kusubu, machukizo kwa Bwana, kazi ya mikono ya fundi, akaisimamisha kwa siri. Na watu wote wajibu, waseme, Amina. 16 Na alaaniwe amdharauye baba yake au mama yake. Na watu wote waseme, Amina. 17 Na alaaniwe aondoaye mpaka wa jirani yake. Na watu wote waseme, Amina. 18 Na alaaniwe ampotezaye kipofu akakosa njia. Na watu wote waseme, Amina. 19 Na alaaniwe apotoaye hukumu ya mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe. Na watu wote waseme, Amina. 20 Na alaaniwe alalaye na mke wa baba yake, kwa kuwa amefunua mavazi ya babaye. Na watu wote waseme, Amina. 21 Na alaaniwe alalaye na mnyama wa aina yo yote. Na watu wote waseme, Amina. 22 Na alaaniwe alalaye na umbu lake, binti ya babaye, au binti ya mamaye. Na watu wote waseme, Amina. 23 Na alaaniwe alalaye na mkwewe, mamaye mkewe. Na watu wote waseme, Amina. 24 Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri. Na watu wote waseme Amina. 25 Na alaaniwe atwaaye ujira wa kumwua asiye makosa. Na watu wote waseme, Amina. 26 Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya. Na watu wote waseme, Amina.

Kumbukumbu la Torati 28

1 Itakuwa utakaposikia sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; 2 na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako. 3 Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani. 4 Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. 5 Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga. 6 Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo. 7 Bwana atawafanya adui zako wainukao juu yako kupigwa mbele yako; watakutokea kwa njia moja, lakini watakimbia mbele yako kwa njia saba. 8 Bwana ataiamuru baraka ije juu yako katika ghala zako, na mambo yote utakayotia mkono wako; naye atakubarikia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako. 9 Bwana atakuweka uwe taifa takatifu kwake, kama alivyokuapia; utakaposhika maagizo ya Bwana, Mungu wako, na kutembea katika njia zake. 10 Na mataifa yote ya duniani watakuona umeitwa kwa jina la Bwana, nao watakuwa na hofu kwako. 11 Bwana atakufanya uwe na wingi wa uheri, katika uzao wa tumbo lako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako, katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako kwamba atakupa. 12 Atakufunulia Bwana hazina yake nzuri, nayo ni mbingu, kwa kutoa mvua ya nchi yako kwa wakati wake, na kwa kubarikia kazi yote ya mkono wako; nawe utakopesha mataifa mengi, wala hutakopa wewe. 13 Bwana atakufanya kuwa kichwa, wala si mkia; nawe utakuwa juu tu, wala huwi chini; utakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wako, nikuagizayo hivi leo, kuyaangalia na kufanya; 14 msipokengeuka katika maneno niwaamuruyo leo kwa lo lote, kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto, kwa kuifuata miungu mingine na kuitumikia. 15 Lakini itakuwa usipotaka kuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, usiyaangalie kufanya maagizo yake yote na amri zake, nikuagizazo hivi leo, ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata. 16 Utalaaniwa mjini, utalaaniwa na mashambani. 17 Litalaaniwa kapu lako na chombo chako cha kukandia. 18 Utalaaniwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. 19 Utalaaniwa uingiapo, utalaaniwa na utokapo, 20 Bwana atakuletea laana na mashaka, na kukemewa, katika yote utakayotia mkono wako kuyafanya, hata uangamie na kupotea kwa upesi; kwa ule uovu wa matendo yako, uliyoniacha kwayo. 21 Bwana atakuambatanisha na tauni, hata atakapokwisha kukuondoa katika nchi uingiayo kwa kuimiliki. 22 Bwana atakupiga kwa kifua kikuu, na kwa homa, na kwa kuwashwa, na kwa hari ya moto, na kwa upanga, na kwa ukaufu, na kwa koga; navyo vitakufukuza hata uangamie. 23 Na mbingu zako zilizo juu ya kichwa chako zitakuwa shaba, na nchi iliyo chini yako itakuwa chuma. 24 Bwana atafanya mvua ya nchi yako iwe vumbi na mchanga; itakujilia juu yako kutoka mbinguni hata uangamie. 25 Bwana atakufanya upigwe mbele ya adui zako; utawatokea juu yao kwa njia moja, lakini utakimbia mbele yao kwa njia saba; nawe utatupwa huko na huko katika falme zote za duniani. 26 Na mzoga wako utakuwa chakula cha ndege wote wa angani, na wanyama wote wa duniani, pasiwe na mtu wa kuwafukuza. 27 Bwana atakupiga kwa majipu ya Misri, na kwa bawasiri, na kwa pele, na kwa kujikuna, ambayo hupati kupoa. 28 Bwana atakupiga kwa wazimu, na kwa upofu, na kwa bumbuazi la moyoni; 29 utakwenda kwa kupapasa-papasa mchana, kama apapasavyo kipofu gizani, wala hufanikiwi katika njia zako; nawe sikuzote utaonewa na kutekwa nyara, wala hapatakuwa na mtu wa kukuokoa. 30 Utaposa mke na mume mwingine atalala naye; utajenga nyumba usiikae; utapanda mizabibu usitumie matunda yake. 31 Ng'ombe wako atachinjwa mbele ya macho yako, usile nyama yake; utanyang'anywa punda wako mbele ya uso wako kwa jeuri, usirudishiwe; kondoo zako watapewa adui zako, usipate mtu wa kukuokoa. 32 Wanao na binti zako litapewa taifa lingine, na macho yako yataangalia, na kuzimia kwa kuwatamani mchana kutwa; wala hapatakuwa na kitu katika uwezo wa mkono wako. 33 Matunda ya nchi yako, na taabu yako yote, vitaliwa na taifa usilolijua; utaonewa tu, na kupondwa chini daima; 34 hata uwe mwenye wazimu kwa yaonwayo na macho yako, utakayoyaona. 35 Bwana atakupiga magoti na miguu kwa jipu lililo zito, usilopata kupozwa, tokea wayo wa mguu mpaka utosi wa kichwa. 36 Bwana atakupeleka wewe, na mfalme wako utakayemweka juu yako, kwa taifa usilolijua wewe wala baba zako; nawe huko utatumikia miungu mingine ya miti na mawe. 37 Nawe utakuwa ushangao, na mithali, na dharau, kati ya mataifa yote huko atakakokuongoza Bwana. 38 Mbegu nyingi utazichukua nje shambani, lakini utavuna haba, kwa kuwa nzige watazila. 39 Utapanda mizabibu na kuitengeza, wala hutakunywa katika divai yake, wala kuichuma kwani italiwa na mabuu. 40 Utakuwa na mizeituni katika mipaka yako yote usijipake mafuta yake; kwa kuwa mzeituni wako utapukutika. 41 Utazaa wana na binti, lakini hawatakuwa wako wewe; kwa sababu watakwenda utumwani. 42 Miti yako yote, na mazao ya nchi yako, nzige watakuwa nayo. 43 Mgeni aliye kati yako atazidi kupaa juu yako; nawe utazidi kushuka chini. 44 Yeye atakukopesha, wala wewe usimkopeshe; yeye atakuwa ni kichwa, wewe utakuwa mkia. 45 Na laana hizi zote zitakujilia juu yako, zitakuandama na kukupata, hata uangamizwe, kwa kuwa hukuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, kushika maagizo yake na amri zake alizokuagiza; 46 nazo zitakuwa juu yako kwa ishara na ajabu, na juu ya uzao wako milele; 47 kwa kuwa hukumtumikia Bwana, Mungu wako, kwa furaha na moyo wa kushukuru, kwa ajili ya ule wingi wa vitu vyote; 48 kwa hiyo utawatumikia adui zako atakaowaleta Bwana juu yako, kwa njaa, na kwa kiu, na kwa uchi, na kwa uhitaji wa vitu vyote; naye atakuvika kongwa la chuma shingoni mwako, hata atakapokwisha kukuangamiza. 49 Bwana atakuletea taifa juu yako kutoka mbali, kutoka ncha ya dunia, kama arukavyo tai; taifa usiloufahamu ulimi wake; 50 taifa lenye uso mkali, ambalo haliangalii uso wa mzee, wala halipendelei kijana; 51 naye atakula uzao wa ng'ombe wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako mpaka utakapokwisha kuangamizwa; wala hatakuachia nafaka, wala divai, wala mafuta, wala maongeo ya ng'ombe wako, wala wana-kondoo wako, hata atakapokwisha kukuangamiza. 52 Naye atakuhusuru katika malango yako yote, hata kuta zako ndefu, zenye maboma, ulizokuwa ukiziamini, zishuke, katika nchi yako yote kila upande; naye atakuhusuru katika malango yako yote kila upande, katika nchi yako yote aliyokupa Bwana, Mungu wako. 53 Nawe utakula uzao wa tumbo lako mwenyewe, nyama ya wana wako na binti zako aliokupa Bwana, Mungu wako; katika mazingirwa na katika mkazo utakaokazwa na adui zako. 54 Mtu mume kati yenu aliye mwororo na laini sana, jicho lake litakuwa ovu juu ya nduguye, na juu ya mke wa kifuani mwake, na juu ya masalio ya wanawe waliosalia naye; 55 hata asitake wao mmojawapo apewe katika nyama ya wanawe atakaowala, kwa kuwa hana kitu kilichomsalia kwake; katika mazingirwa na mkazo utakaokazwa na adui yako katika malango yako yote. 56 Mwanamke kati yenu aliye mwororo na laini, ambaye hangehatirisha kuweka wayo wa mguu wake nchi kwa umalidadi na ulaini, jicho lake huyu litakuwa ovu juu ya mume wa kifuani mwake, na juu ya mwanawe, na juu ya binti yake, 57 na juu ya mchanga wake atokaye katikati ya miguu yake, na juu ya wanawe atakaowazaa; kwa kuwa atawala kwa siri, kwa uhitaji wa vitu vyote; katika mazingirwa na mkazo utakaokazwa na adui yako katika malango yako. 58 Kama hutaki kutunza kufanya maneno yote ya torati hii yaliyoandikwa katika kitabu hiki, upate kulicha jina hili la fahari na utisho, Bwana, MUNGU WAKO; 59 ndipo atakapofanya Bwana mapigo yako yawe ya ajabu, na mapigo ya uzao wako, mapigo makubwa kwa kweli, ya kudumu sana, na magonjwa mazito ya kudumu sana. 60 Naye atakurejezea maradhi yote ya Misri juu yako uliyokuwa ukiyaogopa, nayo yataambatana nawe. 61 Tena kila ugonjwa, na kila pigo yasiyoandikwa katika kitabu cha torati hii, atakutia nayo Bwana juu yako, hata utakapokwisha kuangamizwa. 62 Nanyi mtasalia wachache kwa hesabu, ninyi mliokuwa mfano wa nyota za mbinguni kwa wingi; kwa kuwa hukuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako. 63 Tena itakuwa, kama vile alivyokuwa akifurahi Bwana juu yenu kwa kuwatendea mema na kuwafanya kuwa wengi, ndivyo atakavyofurahi Bwana juu yenu kwa kuwapoteza na kuwaangamiza; nanyi mtanyakuliwa katika hiyo nchi mwingiayo kuimiliki. 64 Bwana atakutawanya katika mataifa yote, tokea ncha hii ya dunia hata ncha hii ya dunia; nawe huko utatumikia miungu mingine usiyoijua wewe wala baba zako, nayo ni miti na mawe. 65 Wala katika mataifa hayo hutapata raha iwayo yote, wala hutakuwa na kituo cha wayo wa mguu wako; lakini Bwana atakupa huko moyo wa kutetema, na macho ya kuzimia, na roho ya kudhoofika; 66 na uzima wako utakuwa na wasiwasi mbele yako; nawe utakuwa na woga usiku na mchana, wala hutaamini kamwe maisha yako; 67 asubuhi utasema, Laiti ingekuwa jioni! Na jioni utasema, Laiti ingekuwa asubuhi! Kwa kicho cha moyo wako utakavyokucha, na kuona kwa macho yako utakavyoona. 68 Bwana atakurudisha tena Misri kwa merikebu, kwa njia ambayo nilikuambia, Hutaiona tena po pote; nanyi huko mtajiuza nafsi zenu kwa adui zenu kuwa watumwa na wajakazi, wala hapana atakayewanunua.

Kumbukumbu la Torati 29

1 Haya ndiyo maneno ya agano Bwana alilomwamuru Musa alifanye na wana wa Israeli katika nchi ya Moabu, pamoja na agano alilofanya nao Horebu. 2 Musa akawaita Israeli wote akawaambia, Mmeyaona yote Bwana aliyomfanya Farao katika nchi ya Misri mbele ya macho yenu, yeye na watumwa wake wote, na nchi yake yote; 3 yale majaribu makuu yaliyoyaona macho yako; hizo ishara, na ile miujiza mikuu; 4 lakini Bwana hakuwapa moyo wa kujua, wala macho ya kuona, wala masikio ya kusikia, hata leo hivi. 5 Nami miaka arobaini nimewaongoza jangwani; nguo zenu hazikuchakaa juu yenu, wala kiatu chako hakikuchakaa katika mguu wako. 6 Hamkula mkate, wala hamkunywa divai, wala kileo; ili mpate kujua kwamba Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 7 Nanyi mlipokuja mahali hapa, walitutokea kupigana juu yetu Sihoni mfalme wa Heshboni, na Ogu mfalme wa Bashani, tukawapiga; 8 tukaitwaa nchi yao, nayo tukawapa Wareubeni, na Wagadi, na nusu ya kabila ya Manase, iwe urithi. 9 Shikeni basi maneno ya agano hili myafanye, ili mfanikiwe katika yote mfanyayo. 10 Leo mmesimama nyote mbele za Bwana, Mungu wenu; wakuu wenu, na kabila zenu, na wazee wenu, na maakida wenu, waume wote wa Israeli, 11 vijana vyenu, na wake wenu, na mgeni wako aliye kati ya kituo chako, tokea mchanjaji wa kuni zako hata mtekaji wa maji yako; 12 ili uingie katika agano la Bwana, Mungu wako, na kiapo chake, afanyacho nawe Bwana, Mungu wako, hivi leo; 13 apate kukuweka leo uwe taifa kwake naye apate kuwa Mungu kwako, kama alivyokuambia, na kama alivyowaapia baba zako, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo. 14 Wala sifanyi na ninyi peke yenu agano hili na kiapo hiki; 15 ila na yeye aliyesimama hapa nasi hivi leo mbele ya Bwana, Mungu wetu, na yeye naye asiyekuwapo pamoja nasi leo; 16 (kwani mwajua mlivyoketi nchi ya Misri, na tulivyo kuja katikati ya mataifa hayo mliyopita katikati yao; 17 nanyi mliona machukizo yao, na sanamu zao, miti na mawe, fedha na dhahabu, zilizokuwako kwao;) 18 asiwe mtu katikati yenu, mume wala mke, wala jamaa, wala kabila, ageukaye moyo wake leo amwache Bwana, Mungu wetu, kwenda kuitumikia miungu ya mataifa hayo; lisiwe katikati yenu shina lizaalo uchungu na pakanga; 19 ikawa asikiapo maneno ya laana hii, ajibarikie mtu huyo moyoni mwake, na kusema, Nitakuwa katika amani, nijapotembea katika upotoe wa moyo wangu kwa kuangamiza mbichi na kavu; 20 Bwana hatamsamehe mtu huyo, lakini wakati huo hasira ya Bwana na wivu wake vitafuka moshi juu ya mtu yule, na laana yote iliyoandikwa katika kitabu hiki itamkalia juu yake, na Bwana atalifuta jina lake chini ya mbingu. 21 Bwana atamtenga kwa uovu, kutoka kabila zote za Israeli, kwa laana zote za agano lililoandikwa katika chuo hiki cha torati. 22 Na kizazi cha baadaye, wanenu watakaoinuka baada yenu, na mgeni atakayekuja kutoka nchi ya mbali, watasema, watakapoyaona mapigo ya nchi ile, na magonjwa aliyoitia Bwana; 23 ya kuwa nchi yake nzima ni kibiriti, na chumvi, na kuteketea, haipandwi, wala haizai, wala nyasi hazimei humo, kama mapinduko ya Sodoma na Gomora, Adma na Seboimu, aliyoipindua Bwana kwa ghadhabu yake na hasira zake; 24 mataifa yote watasema, Mbona Bwana ameifanyia hivi nchi hii? Ni nini maana yake hari ya hasira hizi kubwa? 25 Ndipo watakaposema watu, Ni kwa kuwa waliacha agano la Bwana, Mungu wa baba zao, alilofanya nao hapo alipowatoa katika nchi ya Misri; 26 wakaenda wakatumikia miungu mingine, wakaiabudu miungu wasiyoijua, asiyowapa yeye; 27 ndipo ikawashwa hasira ya Bwana juu ya nchi hii, kwa kuleta juu yake laana yote iliyoandikwa katika kitabu hiki; 28 Bwana akawang'oa katika nchi yao kwa hasira, na ghadhabu, na makamio makuu, akawatupa waende nchi nyingine, kama hivi leo. 29 Mambo ya siri ni ya Bwana, Mungu wetu; lakini mambo yaliyofunuliwa ni yetu sisi na watoto wetu milele, ili tuyafanye maneno yote ya sheria hii.

Kumbukumbu la Torati 30

1 Tena itakuwa, mambo haya yote yatakapokujilia, baraka na laana nilizoweka mbele yako, nawe utakapozikumbuka kati ya mataifa yote, huko atakakokupeleka Bwana, Mungu wako, 2 nawe utakapomrudia Bwana, Mungu wako, na kuitii sauti yake, mfano wa yote nikuagizayo leo, wewe na wanao, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote; 3 ndipo Bwana, Mungu wako, atakapougeuza utumwa wako, naye atakuhurumia, tena atarejea na kukukusanya kutoka mataifa yote, huko alikokutawanyia Bwana, Mungu wako. 4 Watu wako waliotawanyika wakiwako katika ncha za mbingu za mwisho, kutoka huko atakukusanya Bwana, Mungu wako; kutoka huko atakutwaa; 5 atakuleta Bwana, Mungu wako, uingie nchi waliyomiliki baba zako, nawe utaimiliki; naye atakutendea mema, na kukufanya uwe watu wengi kuliko baba zako. 6 Bwana, Mungu wako, atautahiri moyo wako, na moyo wa uzao wako, ili umpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, upate kuwa hai. 7 Na laana hizi zote Bwana, Mungu wako, atawatia adui zako na hao wakuchukiao, waliokuwa wakikutesa. 8 Nawe utarudi, uitii sauti ya Bwana, na kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo. 9 Na Bwana, Mungu wako, atakufanya uwe na wingi wa uheri katika kazi yote ya mkono wako, katika uzao wa tumbo lako, na katika uzao wa ng'ombe wako, na katika uzao wa nchi yako; kwa kuwa Bwana atafurahi tena juu yako kwa wema, kama alivyofurahi juu ya baba zako; 10 ukiwa utaifuata sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa kuyashika maagizo yake, na amri zake zilizoandikwa katika chuo hiki cha torati; ukimwelekea Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote. 11 Kwa maana maagizo haya nikuagizayo leo, si mazito mno kwako, wala si mbali. 12 Si mbinguni, hata useme, Ni nani atakayetupandia mbinguni akatuletee, aje atuambie tusikie, tupate kuyafanya? 13 Wala si ng'ambo ya pili ya bahari, hata useme, Ni nani atakayetuvukia bahari, akatuletee, aje atuambie, tusikie, tupate kuyafanya? 14 Lakini neno li karibu nawe sana, li katika kinywa chako na moyo wako, upate kulifanya. 15 Angalia, nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya; 16 kwa hivi nikuagizavyo leo kumpenda Bwana, Mungu wako, kuenenda katika njia zake, na kushika maagizo yake, na amri zake, na hukumu zake, upate kuwa hai na kuongezeka; Bwana, Mungu wako, apate kukubarikia katika nchi uingiayo kuimiliki. 17 Lakini moyo wako ukikengeuka, usipotaka kusikiza, lakini ukavutwa kando kwenda kuabudu miungu mingine, na kuitumikia; 18 nawahubiri hivi leo hakika mtaangamia; hamtazifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi, uivukiayo Yordani, uingie kuimiliki. 19 Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; 20 kumpenda Bwana, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako; upate kukaa katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kuwa atawapa.

Kumbukumbu la Torati 31

1 Musa akaenda akawaambia Waisraeli maneno haya yote. 2 Akawaambia, Mimi leo ni mwenye miaka mia na ishirini; siwezi tena kutoka na kuingia, na Bwana ameniambia, Hutavuka mto huu Yordani. 3 Bwana Mungu wako, ndiye atakayevuka mbele yako, atawaangamiza mataifa haya mbele yako, nawe utawamiliki; na Yoshua atavuka mbele yako, kama Bwana alivyonena. 4 Na Bwana atawatenda hao kama vile alivyowatenda Sihoni na Ogu, wafalme wa Waamori, na nchi yao, ambao aliwaharibu. 5 Naye Bwana atawatia mikononi mwenu, nanyi mtawatenda kadiri ya amri ile niliyowaamuru. 6 Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana Bwana, Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha. 7 Musa akamwita Yoshua, akamwambia machoni pa Israeli wote, Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana utakwenda pamoja na watu hawa hata nchi Bwana aliyowaapia baba zao, ya kwamba atawapa; nawe utawarithisha. 8 Naye Bwana, yeye ndiye atakayekutangulia, atakuwa pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha; usiogope wala usifadhaike. 9 Musa akaiandika torati hii, akawapa makuhani, wana wa Lawi, waliolichukua sanduku la agano la Bwana, na wazee wote wa Israeli. 10 Musa, akawaamuru, akasema, Mwisho wa kila mwaka wa saba, wakati wa maachilio, wakati ulioamriwa wa sikukuu ya vibanda, 11 Israeli wote wafikapo ili kuonekana mbele za Bwana, Mungu wako, mahali pale atakapopachagua, uisome torati hii mbele ya Israeli wote masikioni mwao. 12 Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni wako aliyemo malangoni mwako wapate kusikia na kujifunza, na kumcha Bwana, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii; 13 na watoto wao wasiojua, wapate kusikia na kujifunza kumcha Bwana, Mungu wenu, siku zote mtakazokaa katika nchi mnayoivukia Yordani ili kuimiliki. 14 Bwana akamwambia Musa, Tazama, siku zako za kufa zinakaribia, umwite Yoshua, nanyi mkajihudhurishe katika hema ya kukutania, ili nipate kumwagiza kazi. Musa na Yoshua wakaenda, wakajihudhurisha ndani ya hema ya kukutania. 15 Bwana akaonekana katika Hema katika nguzo ya wingu; na ile nguzo ya wingu ikasimama juu ya mlango wa Hema. 16 Bwana akamwambia Musa, Angalia, wewe utalala na baba zako; na watu hawa wataondoka, wataifuata kwa ukahaba miungu ya kigeni ya nchi waiendeayo kuwa kati yao, nao wataniacha mimi na kulivunja agano langu, nililofanya nao. 17 Ndipo hasira yangu itakapowaka juu yao siku hiyo, nami nitawaacha, nitawaficha uso wangu, nao wataliwa, tena watajiliwa na mambo maovu mengi na mashaka; hata waseme siku hiyo, Je! Kujiliwa kwetu na maovu haya si kwa sababu Mungu wetu hayumo kati yetu? 18 Nami nitawaficha uso wangu kwa kweli siku hiyo, kwa maovu yote waliyoyafanya, kwa kuigeukia hiyo miungu mingine. 19 Basi sasa jiandikieni wimbo huu, uwafundishe wana wa Israeli; kawatie vinywani mwao, ili uwe shahidi kwangu wimbo huu, juu ya wana wa Israeli. 20 Kwa kuwa nitakapokwisha kuwatia katika nchi niliyowaapia baba zao, imiminikayo maziwa na asali; nao watakapokwisha kula na kushiba, na kuwanda; ndipo watakapoigeukia hiyo miungu mingine, na kuitumikia, na kunidharau mimi, na kulivunja agano langu. 21 Tena itakuwa, wakiisha kujiliwa na mambo maovu mengi na mashaka, utashuhudia wimbo huu mbele yao kama shahidi, kwa maana hautasahauliwa katika vinywa vya uzao wao; kwani nayajua mawazo yao wayawazayo, hata sasa kabla sijawatia katika nchi niliyoapa. 22 Basi Musa akauandika wimbo huu siku iyo hiyo, akawafundisha wana wa Israeli. 23 Akamwagiza Yoshua, mwana wa Nuni, akamwambia, Uwe hodari na moyo mkuu, kwa kuwa utawapeleka wana wa Israeli katika nchi niliyowaapia; nami nitakuwa pamoja nawe. 24 Basi ikawa hapo Musa alipomaliza kuandika maneno ya torati hii katika chuo, hata yakaisha, 25 ndipo Musa akawaamuru Walawi waliokuwa wakilichukua sanduku la agano la Bwana akawaambia, 26 Twaeni chuo hiki cha torati, mkiweke kando ya sanduku la agano la Bwana, Mungu wenu, ili kiwepo kama shahidi juu yako. 27 Kwa kuwa uasi wako naujua, na shingo yako ngumu; angalieni, mimi nikali hai pamoja nanyi leo, mmekuwa waasi juu ya Bwana; siuze nitakapokwisha kufa! 28 Nikutanishieni wazee wote wa kabila zenu, na maakida yenu, ili niseme maneno haya masikioni mwao, na kuwashuhudizia mbingu na nchi juu yao. 29 Kwa sababu najua baada ya kufa kwangu mtajiharibu kabisa, na kukengeuka katika njia niliyowaamuru; nayo mabaya yatawapata siku za mwisho, kwa vile mtakavyofanya maovu machoni pa Bwana kumtia kasirani kwa kazi ya mikono yenu. 30 Musa akasema maneno ya wimbo huu masikioni mwa kusanyiko la wana wa Israeli hata yakaisha.

Kumbukumbu la Torati 32

1 Kumbukumbu la Torati, Chapter :Sikilizeni, enyi mbingu, nami nitanena; Na nchi isikie maneno ya kinywa changu. 2 Mafundisho yangu yatadondoka kama mvua, Maneno yangu yatatona-tona kama umande; Kama manyunyu juu ya majani mabichi; Kama matone ya mvua juu ya mimea. 3 Maana nitalitangaza Jina la Bwana; Mpeni ukuu Mungu wetu. 4 Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; Maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili. 5 Wametenda mambo ya uharibifu, Hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao; Wao ni kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka. 6 Je! Mnamlipa Bwana hivi, Enyi watu wapumbavu na ujinga? Je! Yeye siye baba yako aliyekununua? Amekufanya, na kukuweka imara. 7 Kumbuka siku za kale, Tafakari miaka ya vizazi vingi; Mwulize baba yako, naye atakuonyesha; Wazee wako, nao watakuambia. 8 Yeye Aliye Juu alipowapa mataifa urithi wao, Alipowabagua wanadamu, Aliweka mipaka ya watu Kwa kadiri ya hesabu ya wana wa Israeli. 9 Maana, sehemu ya Bwana ni watu wake, Yakobo ni kura ya urithi wake. 10 Alimkuta katika nchi ya ukame, Na katika jangwa tupu litishalo; Alimzunguka, akamtunza; Akamhifadhi kama mboni ya jicho; 11 Mfano wa tai ataharikishaye kioto chake; Na kupapatika juu ya makinda yake, Alikunjua mbawa zake, akawatwaa, Akawachukua juu ya mbawa zake; 12 Bwana peke yake alimwongoza, Wala hapakuwa na mungu mgeni pamoja naye. 13 Alimpandisha mahali pa nchi palipoinuka, Naye akala mazao ya mashamba; Akamnyonyesha asali iliyotoka jabalini, Na mafuta yaliyotoka katika mwamba wa gumegume; 14 Siagi ya ng'ombe, na maziwa ya kondoo, Pamoja na mafuta ya wana-kondoo, Kondoo waume wa Kibashani, na mbuzi, Na unono wa ngano iliyo nzuri; Ukanywa divai, damu ya mizabibu. 15 Lakini Yeshuruni alinenepa, akapiga teke; Umenenepa, umekuwa mnene, umewanda; Ndipo akamwacha Mungu aliyemfanya, Akamdharau Mwamba wa wokovu wake. 16 Wakamtia wivu kwa miungu migeni, Wakamkasirisha kwa machukizo. 17 Walitoa sadaka kwa pepo, si Mungu, Kwa miungu wasiyoijua, Kwa miungu mipya iliyotokea siku zilizo karibu, Ambayo baba zenu hawakuiogopa. 18 Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa, Mungu aliyekuzaa umemsahau. 19 Bwana akaona, akawachukia, Kwa sababu ya kukasirishwa na wanawe na binti zake. 20 Akasema, Nitawaficha uso wangu, Nitaona mwisho wao utakuwaje; Maana, ni kizazi cha ukaidi mwingi, Watoto wasio imani ndani yao. 21 Wamenitia wivu kwa kisicho Mungu; Wamenikasirisha kwa ubatili wao; Nami nitawatia wivu kwa wasio watu, Nami nitawakasirisha kwa taifa lipumbaalo. 22 Maana, moto umewashwa kwa hasira yangu, Unateketea hata chini ya kuzimu, Unakula dunia pamoja na mazao yake, Unaunguza misingi ya milima. 23 Nitaweka madhara juu yao chunguchungu; Nitawapiga kwa mishale yangu hata ikaishe; 24 Watakonda kwa njaa, wataliwa na makaa ya moto, Na uharibifu mkali; Nitawapelekea meno ya wanyama wakali, Pamoja na sumu ya wadudu watambaao mavumbini. 25 Nje upanga utawafifiliza Na ndani ya vyumba, utisho; Utaangamiza mvulana na msichana, Anyonyaye pamoja na mwenye mvi, 26 Nalisema, Ningewatawanyia mbali, Ningekomesha kumbukumbu lao kati ya wanadamu; 27 Isipokuwa naliogopa makamio ya adui, Adui zao wasije wakafikiri uongo, Wasije wakasema, Mkono wetu umetukuka, Wala Bwana hakuyafanya haya yote. 28 Maana hawa ni taifa wasio shauri, Wala fahamu hamna ndani yao. 29 Laiti wangekuwa na akili, hata wakafahamu haya, Ili watafakari mwisho wao. 30 Mmoja angefukuzaje watu elfu, Wawili wangekimbizaje elfu kumi, Kama Mwamba wao asingaliwauza, Kama Bwana asingaliwatoa? 31 Maana, Mwamba wao si kama Mwamba wetu, Hata adui zetu wenyewe ndivyo wahukumuvyo. 32 Maana, mzabibu wao ni mzabibu wa Sodoma, Nao ni wa mashamba ya Gomora; Zabibu zao ni zabibu za uchungu, Vichala vyao ni vichungu. 33 Mvinyo yao ni sumu ya majoka, Uchungu mkali wa nyoka. 34 Je! Haya hayakuwekwa akiba kwangu? Na kutiwa muhuri kati ya hazina yangu? 35 Kisasi ni changu mimi, na kulipa, Wakati itakapoteleza miguu yao; Maana siku ya msiba wao imekaribia, Na mambo yatakayowapata yatafanya haraka. 36 Kwa kuwa Bwana atawaamua watu wake, Atawahurumia watumwa wake, Aonapo ya kuwa nguvu zao zimeondoka, Na ya kuwa habaki mtu, aliyefungwa wala asiyefungwa, 37 Naye atasema, Iko wapi miungu yao, Mwamba ule walioutumaini; 38 Uliokula shahamu za sadaka zao, Na kunywa divai ya sadaka zao za kinywaji? Na waondoke na kuwasaidia ninyi; Na wawe hao himaya yenu. 39 Fahamu sasa ya kuwa Mimi, naam, Mimi ndiye, Wala hapana Mungu mwingine ila Mimi; Naua Mimi, nahuisha Mimi, Nimejeruhi, tena naponya; Wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu, 40 Maana, nainua mkono wangu mbinguni, Na kusema, Kama Mimi niishivyo milele, 41 Nikiunoa upanga wangu wa umeme, Mkono wangu ukishika hukumu, Nitawatoza kisasi adui zangu, Nitawalipa wanaonichukia. 42 Nitailevya mishale yangu kwa damu, Na upanga wangu utakula nyama; Pamoja na damu ya waliouawa na waliotekwa nyara, Katika vichwa vya wakuu wa adui. 43 Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake; Kwa maana atatwaa kisasi kwa damu ya watumwa wake, Atawatoza kisasi adui zake, Tena atafanya kafara kwa nchi yake, na watu wake. 44 Musa akaja akasema maneno haya yote ya wimbo huu masikioni mwa watu, yeye na Yoshua, mwana wa Nuni. 45 Musa akamaliza kuwaambia Israeli wote maneno haya yote; 46 akawaambia, Yawekeni mioyoni mwenu maneno yote ambayo nashuhudia kwenu hivi leo; nayo waamuruni watoto wenu, wayatunze na kuyafanya maneno yote ya torati hii. 47 Kwa maana si jambo lisilofaa kwenu; maana, ni maisha yenu, na kwa jambo hili mtazifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi mwivukiayo Yordani kuimiliki. 48 Bwana akasema na Musa siku iyo hiyo, akamwambia, 49 Kwea katika mlima huu wa Abarimu, mpaka kilima cha Nebo, kilicho katika nchi ya Moabu, kuelekea Yeriko; ukaangalie nchi ya Kanaani niwapayo wana wa Israeli kuimiliki; 50 ukafe katika kilima, huko ukweako, ukusanywe uwe pamoja na jamaa zako; kama alivyokufa nduguyo Haruni katika mlima wa Hori, akakusanywa awe pamoja na watu wake; 51 kwa sababu mlinikosa ninyi juu yangu katikati ya wana wa Israeli katika maji ya Meriba huko Kadeshi, katika bara ya Sini; kwa kuwa hamkunitakasa katikati ya wana wa Israeli. 52 Kwani utaiona hiyo nchi mbele yako, lakini hutakwenda huko kuingia hiyo nchi niwapayo wana wa Israeli.

Kumbukumbu la Torati 33

1 Kumbukumbu la Torati, Chapter :Hii ndiyo baraka ya Musa, huyo mtu wa Mungu, aliyowabarikia wana wa Israeli kabla ya kufa kwake. 2 Akasema,Bwana alitoka Sinai,Akawaondokea kutoka Seiri;Aliangaza katika kilima cha Parani,Akaja Meribath-Kadeshi.Upande wake wa kuume Palikuwa na sheria ya moto-moto kwao. 3 Hakika awapenda hayo makabila ya watu; Watakatifu wake wote wamo mkononi mwako; Nao waliketi miguuni pako; Watapokea kila mmoja katika maneno yako. 4 Musa alituagiza torati, Ni urithi kwa mkutano wa Yakobo. 5 Akawa mfalme katika Yeshuruni, Walipokutanika wakuu wa watu, Makabila yote ya Israeli pamoja. 6 Reubeni na aishi, asife; Lakini watu wake na wawe wachache. 7 Na baraka ya Yuda ni hii; akasema, Isikize, Ee Bwana, sauti ya Yuda, Umlete ndani kwa watu wake; Alijitetea kwa mikono yake; Nawe utakuwa msaada juu ya adui zake. 8 Akamnena Lawi, Thumimu yako na Urimu yako vina mtakatifu wako, Uliyemjaribu huko Masa; Ukateta naye kwenye maji ya Meriba. 9 Aliyemtaja baba yake na mama yake, Mimi sikumwona; Wala nduguze hakuwakubali; Wala hakuwajua watoto wake mwenyewe; Maana wameliangalia neno lako, Wamelishika agano lako. 10 Watamfundisha Yakobo hukumu zako, Na Israeli torati yako, Wataweka uvumba mbele zako, Na sadaka nzima za kuteketezwa madhabahuni mwako. 11 Ee Bwana, ubariki mali zake, Utakabali kazi ya mikono yake; Uwapige viuno vyao waondokao juu yake, Na wenye kumchukia, wasiinuke tena. 12 Akamnena Benyamini, Mpenzi wa Bwana atakaa salama kwake; Yuamfunika mchana kutwa, Naye hukaa kati ya mabega yake. 13 Na Yusufu akamnena, Nchi yake na ibarikiwe na Bwana; Kwa vitu vya thamani vya mbinguni, kwa huo umande, Na kwa kilindi kilalacho chini, 14 Na kwa vitu vilivyo bora vya matunda ya jua, Na kwa vitu vilivyo bora vya maongeo ya miezi, 15 Na kwa vitu viteule vya milima ya kale, Na kwa vitu vilivyo bora vya vilima vya milele, 16 Na kwa vitu vilivyo bora vya nchi, na kujaa kwake, Na uradhi wake aliyekaa ndani ya kile kijiti; Na ije baraka juu ya kichwa chake Yusufu, Juu ya utosi wa kichwa chake aliyetengwa na nduguze. 17 Mzaliwa wa kwanza wa ng'ombe wake mume, enzi ni yake; Na pembe zake ni pembe za nyati; Kwa hizo atayasukuma mataifa yote, hata ncha za nchi; Nao ni makumi ya maelfu ya Efraimu, Nao ni maelfu ya Manase. 18 Na Zabuloni akamnena, Furahi Zabuloni, katika kutoka kwako; 19 Watayaita mataifa waje mlimani; Wakasongeze huko sadaka za haki; Kwa kuwa watanyonya wingi wa bahari, Na akiba zilizofichamana za mchangani. 20 Na Gadi akamnena, Na abarikiwe amwongezaye Gadi; Yeye hukaa kama simba mke, Hurarua mkono, naam, na utosi wa kichwa. 21 Akajichagulia sehemu ya kwanza, Kwani ndiko lilikowekwa fungu la mtoa-sheria; Akaja pamoja na wakuu wa watu, Akaitekeleza haki ya Bwana, Na hukumu zake kwa Israeli. 22 Na Dani akamnena, Dani ni mwana-simba, Arukaye kutoka Bashani. 23 Na Naftali akamnena, Ee Naftali, uliyeshiba fadhili, Uliyejawa na baraka ya Bwana; Umiliki magharibi na kusini. 24 Na Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta. 25 Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba; Na kadiri ya siku zako ndivyo zitakavyokuwa nguvu zako. 26 Hapana aliyefanana na Mungu, Ee Yeshuruni, Ajaye amepanda juu ya mbingu ili akusaidie. Na juu ya mawingu katika utukufu wake. 27 Mungu wa milele ndiye makazi yako, Na mikono ya milele i chini yako. Na mbele yako amemsukumia mbali adui; Akasema, Angamiza. 28 Na Israeli anakaa salama, Chemchemi ya Yakobo peke yake, Katika nchi ya ngano na divai; Naam, mbingu zake zadondoza umande. 29 U heri, Israeli. Ni nani aliye kama wewe, taifa lililookolewa na Bwana! Ndiye ngao ya msaada wako, Na upanga wa utukufu wako; Na adui zako watajitiisha chini yako, Nawe utapakanyaga mahali pao pa juu.

Kumbukumbu la Torati 34

1 Musa akapanda kutoka uwanda wa Moabu mpaka mlima Nebo, hata kilele cha Pisga kukabili Yeriko. Bwana akamwonyesha nchi yote ya Gileadi hata Dani; 2 na Naftali yote, na nchi ya Efraimu na Manase, na nchi yote ya Yuda, mpaka bahari ya magharibi; 3 na Negebu, na uwanja wa bonde la Yeriko, mji wa mitende, hata mpaka Soari. 4 Bwana akamwambia, Hii ndiyo nchi niliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, nikisema, Nitawapa wazao wako. Basi nimekuonyesha kwa macho yako, lakini hutavuka huko. 5 Basi Musa, mtumishi wa Bwana, akafa huko, katika nchi ya Moabu, kwa neno la Bwana. 6 Akamzika bondeni, katika nchi ya Moabu, kukabili Beth-peori; lakini hapana mtu ajuaye kaburi lake hata leo. 7 Musa alikuwa mtu wa miaka mia na ishirini alipokufa; jicho lake halikupofuka, wala nguvu za mwili wake hazikupunguka. 8 Wana wa Israeli wakamwombolezea Musa katika uwanda wa Moabu siku thelathini; basi siku za maombolezo ya matanga ya Musa zikaisha. 9 Na Yoshua, mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama Bwana alivyomwamuru Musa. 10 Wala hajainuka tena katika Israeli nabii kama Musa, ambaye Bwana alimjua uso kwa uso; 11 katika ishara zote na maajabu yote, ambayo Bwana alimtuma kuyatenda katika nchi ya Misri, kwa Farao, na kwa watumishi wake wote, na kwa nchi yake yote; 12 na katika ule mkono wa nguvu wote, tena katika ule utisho mkuu wote, alioutenda Musa machoni pa Israeli wote.

Yoshua 1

1 Ikawa baada ya kufa kwake Musa, mtumishi wa Bwana, Bwana akamwambia Yoshua, mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa, akasema, 2 Musa mtumishi wangu amekufa; haya basi, ondoka, vuka mto huu wa Yordani; wewe na watu hawa wote, mkaende hata nchi niwapayo wana wa Israeli. 3 Kila mahali zitakapopakanyaga nyayo za miguu yenu, nimewapa ninyi, kama nilivyomwapia Musa. 4 Tangu jangwa hili na mlima huu, Lebanoni, mpaka mto ule mkubwa, mto wa Frati, nchi yote ya Wahiti, tena mpaka bahari ile kubwa upande wa machweo ya jua, hapo ndipo patakapokuwa mpaka wenu. 5 Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha. 6 Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa. 7 Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. 8 Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana. 9 Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako. 10 Ndipo Yoshua akawaamuru maakida wa watu, akisema, 11 Piteni katikati ya matuo, mkawaamuru hao watu, mkisema, Fanyeni tayari vyakula; kwa maana baada ya siku tatu mtavuka mto huu wa Yordani, ili kuingia na kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wenu, mpate kuimiliki. 12 Tena Yoshua akawaambia Wareubeni, na Wagadi, na hao wa nusu ya kabila ya Manase, akasema, 13 Likumbukeni neno lile alilowaamuru Musa mtumishi wa Bwana, akisema, Bwana, Mungu wenu, anawapa ninyi raha, naye atawapa nchi hii. 14 Wake zenu, na watoto wenu, na makundi yenu, watakaa katika nchi aliyowapa Musa ng'ambo ya Yordani; bali ninyi mtavuka mbele ya ndugu zenu, hali mmevikwa silaha zenu, watu wote wenye nguvu, na ushujaa, ili mpate kuwasaidia; 15 hata Bwana atakapowapa ndugu zenu raha, kama alivyowapa ninyi, na wao pia wamepata kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wenu; ndipo mtakapoirudia nchi ya milki yenu na kuimiliki, ambayo Musa mtumishi wa Bwana aliwapeni ng'ambo ya Yordani upande wa maawio ya jua. 16 Wakamjibu Yoshua, wakasema, Hayo yote uliyotuamuru tutayafanya, na kila mahali utakakotutuma tutakwenda. 17 Kama vile tulivyomsikiliza Musa katika mambo yote, ndivyo tutakavyokusikiliza wewe; Bwana, Mungu wako, na awe pamoja nawe tu, kama alivyokuwa pamoja na Musa. 18 Kila mtu atakayeiasi amri yako, asiyasikilize maneno yako katika mambo yote utakayomwamuru, atauawa. Uwe hodari na moyo wa ushujaa, hilo tu.

Yoshua 2

1 Yoshua, mwana wa Nuni, akawatuma watu wawili kutoka Shitimu kwa siri, ili kupeleleza, akawaambia, Enendeni mkaitazame nchi hii, na Yeriko. Wakaenda wakafika nyumbani kwa kahaba mmoja jina lake aliitwa Rahabu, wakalala huko. 2 Mfalme wa Yeriko akaambiwa, kusema, Tazama, watu wawili wa wana wa Israeli wameingia humu leo usiku, ili kuipeleleza nchi. 3 Mfalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akasema, Watoe watu wale waliokuja kwako, walioingia ndani ya nyumba yako, maana wamekuja ili kuipeleleza nchi. 4 Yule mwanamke akawatwaa wale watu wawili, akawaficha, akasema, Naam, wale watu walikuja kwangu, lakini sikujua walikotoka; 5 ikawa kama wakati wa kufungwa lango la mji, kulipokuwa giza, watu wale wakatoka, wala sijui walikokwenda; wafuateni upesi, maana mtawapata. 6 Lakini yeye alikuwa amewapandisha darini, akawaficha kwa mabua ya kitani, aliyokuwa ameyatandika juu ya dari. 7 Basi hao watu wakawafuata kwa njia iendayo Yordani mpaka vivukoni; na mara wale watu waliowafuatia walipokwisha kutoka, wakalifunga lango. 8 Tena kabla hawajalala akawaendea juu darini, 9 akawaambia wale wanaume, Mimi najua ya kuwa Bwana amewapa ninyi nchi hii, na ya kuwa hofu imetuangukia mbele yenu, na ya kuwa wenyeji wote wa nchi wanayeyuka mbele yenu. 10 Maana tumesikia jinsi Bwana alivyoyakausha maji ya bahari ya Shamu mbele yenu, hapo mlipotoka Misri, tena mambo hayo mliyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa huko ng'ambo ya Yordani, yaani, Sihoni na Ogu, mliowaangamiza kabisa. 11 Na mara tuliposikia hayo mioyo yetu iliyeyuka, wala haukusalia ujasiri wo wote katika mtu awaye yote, kwa sababu yenu; kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, yeye ndiye Mungu, katika mbingu juu na katika nchi chini. 12 Basi sasa, nawasihi, niapieni kwa Bwana, kwa kuwa nimewatendea ihisani, ya kwamba ninyi nanyi mtaitendea ihisani nyumba ya baba yangu; tena nipeni alama ya uaminifu; 13 ya kwamba mtawaponya hai baba yangu na mama yangu, na ndugu zangu wanaume na wanawake, na vitu vyote walivyo navyo, na kutuokoa roho zetu na kufa. 14 Wale wanaume wakamwambia, Uhai wetu badala ya uhai wenu, ikiwa hamwitangazi habari ya shughuli yetu hii; kisha itakuwa, wakati Bwana atakapotupa nchi hii, tutakutendea kwa ihisani na uaminifu. 15 Ndipo akawashusha kwa kamba dirishani, maana nyumba yake ilikuwa katika ukuta wa mji; naye alikaa ukutani. 16 Akawaambia, Enendeni zenu mlimani, wale wanaowafuatia wasije wakawapata; mkajifiche huko siku tatu hata wao wanaowafuatia watakaporudi; kisha enendeni zenu. 17 Wale wanaume wakamwambia, Sisi tunataka tusiwe na hatia kwa ajili ya kiapo hiki ulichotuapisha. 18 Angalia, tutakapoingia katika nchi hii, funga kamba hii nyekundu katika dirisha hili ulilotutelemshia; nawe uwakusanye kwako nyumbani mwako, baba yako, na mama yako, na ndugu zako, na watu wote wa nyumba ya baba yako. 19 Itakuwa mtu awaye yote atakayetoka katika mlango wa nyumba yako kwenda njiani, damu yake itakuwa juu ya kichwa chake mwenyewe, na sisi tutakuwa hatuna hatia; na mtu atakayekuwa ndani ya nyumba yako damu yake itakuwa juu ya vichwa vyetu, mkono wa mtu ukimpata. 20 Lakini wewe ukitangaza habari yetu hii, ndipo tutakuwa hatuna hatia, katika kiapo hiki ulichotuapisha. 21 Naye akasema, Na iwe hivyo kama yalivyo maneno yenu. Akawatoa, nao wakaenda zao; naye akaifunga ile kamba nyekundu dirishani 22 Watu hao wakaenda, wakafika mlimani, wakakaa huko siku tatu, hata wale waliowafuatia walipokuwa wamerudi; na wale waliowafuatia wakawafuatia katika njia ile yote, lakini hawakuwaona. 23 Kisha wale watu wakarudi, wakatelemka mlimani, wakavuka, wakamwendea Yoshua, mwana wa Nuni, nao wakamwambia habari za mambo yote yaliyowapata. 24 Wakamwambia Yoshua, Hakika Bwana ameitia nchi yote katika mikono yetu; tena zaidi ya hayo wenyeji wa nchi wanayeyuka mbele yetu.

Yoshua 3

1 Yoshua akaondoka asubuhi na mapema, nao wakatoka Shitimu, wakafika mto wa Yordani, yeye na wana wa Israeli wote, wakakaa hapo kabla ya kuvuka. 2 Ikawa baada ya siku tatu, maakida wakapita katikati ya marago, 3 wakawaamuru watu wote wakisema, Mtakapoliona sanduku la agano la Bwana, Mungu wenu, na makuhani Walawi wakilichukua, ndipo mtakapoondoka hapa mlipo na kulifuata. 4 Lakini, na iwe nafasi kati ya ninyi na lile sanduku, kama dhiraa elfu mbili kiasi chake; msilikaribie mpate kuijua njia ambayo hamna budi kuiendea; kwa maana hamjapita njia hii bado. 5 Yoshua akawaambia watu, Jitakaseni; maana kesho Bwana atatenda mambo ya ajabu kati yenu. 6 Kisha Yoshua akawaambia makuhani, akasema, Liinueni sanduku la agano, mkavuke mbele ya hao watu. Wakaliinua sanduku la agano, wakatangulia mbele ya watu. 7 Bwana akamwambia Yoshua, Hivi leo nitaanza kukutukuza mbele ya Israeli wote, wapate kujua ya kuwa mimi nitakuwa pamoja na wewe, kama nilivyokuwa pamoja na Musa. 8 Nawe uwaamuru hao makuhani walichukuao sanduku la agano, ukawaambie, Mtakapofika ukingo wa maji ya Yordani, simameni katika Yordani. 9 Basi Yoshua akawaambia wana wa Israeli, Njoni huku, mkayasikie maneno ya Bwana, Mungu wenu. 10 Yoshua akasema, Kwa jambo hili mtajua ya kuwa Mungu aliye hai yu kati yenu, na ya kuwa hatakosa kuwatoa mbele yenu Mkanaani, na Mhiti, na Mhivi, na Mperizi, na Mgirgashi, na Mwamori, na Myebusi. 11 Tazama, sanduku la agano la Bwana wa dunia yote linavuka mbele yenu na kuingia Yordani. 12 Basi sasa twaeni watu kumi na wawili katika kabila za Israeli, kila kabila mtu mmoja. 13 Itakuwa, wakati nyayo za makuhani walichukuao sanduku la Bwana, Bwana wa dunia yote, zitakaposimama katika maji ya Yordani, hayo maji ya Yordani yatatindika, maji yale yashukayo kutoka juu; nayo yatasimama kama chuguu. 14 Hata ikawa, hao watu walipotoka katika hema zao, ili kuvuka Yordani, makuhani waliolichukua sanduku la agano wakatangulia mbele ya watu, 15 basi hao waliolichukua hilo sanduku walipofika Yordani, na nyayo za makuhani waliolichukua sanduku zilipotiwa katika maji ya ukingoni, (maana Yordani hujaa hata kingo zake na kufurika wakati wote wa mavuno), 16 ndipo hayo maji yaliyoshuka kutoka juu yakasimama, yakainuka, yakawa chuguu, mbali sana, huko Adamu, mji ule ulio karibu na Sarethani, na maji yale yaliyotelemkia bahari ya Araba, yaani Bahari ya Chumvi, yakatindika kabisa; watu wakavuka kukabili Yeriko. 17 Na hao makuhani waliolichukua sanduku la agano la Bwana wakasimama imara mahali pakavu katikati ya Yordani; Israeli wote wakavuka katika nchi kavu, hata taifa lile lote likaisha kuvuka Yordani.

Yoshua 4

1 Ikawa, hapo hilo taifa zima lilipokuwa limekwisha vuka Yordani, ndipo Bwana akanena na Yoshua, akamwambia, 2 Haya, twaeni watu waume kumi na wawili katika hao watu, kila kabila mtu mmoja, 3 kisha uwaamrishe, kusema, Twaeni mawe kumi na mawili, hapo katikati ya Yordani, mahali hapo miguu ya hao makuhani iliposimama imara, mwende nayo mawe hayo, mkayaweke nchi kambini, hapo mtakapolala usiku huu. 4 Basi Yoshua akawaita hao watu kumi na wawili, aliokuwa amewaweka tayari tangu hapo, katika wana wa Israeli, kila kabila mtu mmoja; 5 naye Yoshua akawaambia, Haya, piteni ninyi mtangulie mbele ya sanduku la Bwana, Mungu wenu, mwende pale katikati ya Yordani, mkatwae kila mtu wenu jiwe moja begani mwake, kwa kadiri ya hesabu ya kabila za wana wa Israeli; 6 ili kwamba jambo hili liwe ishara kati yenu, hapo watoto wenu watakapowauliza ninyi katika siku zijazo, wakisema, Ni nini maana yake mawe haya? 7 Ndipo mtakapowaambia, Ni kwa sababu maji ya Yordani yalitindika mbele ya sanduku la agano la Bwana; hapo lilipovuka Yordani, hayo maji ya Yordani yalitindika; na mawe haya yatakuwa ni ukumbusho kwa wana wa Israeli milele. 8 Basi wana wa Israeli walifanya vile vile kama Yoshua alivyowaamuru, nao wakatwaa mawe kumi na mawili pale katikati ya Yordani, kama Bwana alivyomwambia Yoshua, sawasawa na hesabu ya kabila za wana wa Israeli; wakayachukua wakavuka nayo hata mahali pale walipolala, nao wakayaweka nchi kuko huko. 9 Kisha Yoshua akapanga mawe kumi na mawili katikati ya Yordani, mahali pale miguu ya hao makuhani waliolichukua hilo sanduku la agano iliposimama; nayo yapo pale pale hata hivi leo. 10 Kwa kuwa makuhani waliolichukua hilo sanduku walisimama katikati ya Yordani, hata mambo yote Bwana aliyomwamuru Yoshua awambie hao watu yakaisha, sawasawa na hayo yote Musa aliyokuwa amemwamuru Yoshua; kisha hao watu wakafanya haraka wakavuka. 11 Ikawa watu wote walipokuwa wamekwisha vuka kabisa, hilo sanduku la Bwana likavuka, na hao makuhani, mbele ya macho ya hao watu. 12 Na wana wa Reubeni, na wana wa Gadi na hiyo nusu ya kabila ya Manase, wakavuka, hali ya kuvaa silaha mbele ya wana wa Israeli, kama Musa alivyowaambia; 13 walipata kama watu arobaini elfu hesabu yao, wenye kuvaa silaha tayari kwa vita, waliovuka mbele ya Bwana, waende vitani, hata nchi tambarare za Yeriko. 14 Siku ile Bwana alimtukuza Yoshua mbele ya macho ya Israeli wote; nao wakamcha, kama walivyokuwa wakimcha Musa, siku zote za maisha yake. 15 Kisha Bwana akanena na Yoshua, akamwambia, 16 Haya, uwaamuru makuhani, hao waliolichukua sanduku la ushuhuda, kwamba wakwee juu kutoka mle katika Yordani. 17 Basi Yoshua akawaamuru hao makuhani, akawaambia, Haya, kweeni mtoke Yordani. 18 Ilikuwa, hapo hao makuhani waliolichukua sanduku la agano la Bwana walipokwea juu kutoka mle kati ya Yordani, na nyayo za miguu yao hao makuhani zilipoinuliwa na kutiwa katika nchi kavu, ndipo maji ya Yordani yaliporudi mahali pake, na kujaa na kuipita mipaka yake, kama yalivyokuwa hapo kwanza. 19 Na hao watu wakakwea kutoka Yordani siku ya kumi ya mwezi wa kwanza, wakapiga kambi Gilgali, katika mpaka wa mashariki wa Yeriko. 20 Na yale mawe kumi na mawili waliyoyatwaa katikati ya Yordani Yoshua akayasimamisha Gilgali. 21 Akawaambia wana wa Israeli, akasema, Watoto wenu watakapowauliza baba zao katika siku zijazo, wakisema, Mawe haya maana yake ni nini? 22 Ndipo mtakapowaarifu watoto wenu mkisema, Israeli walivuka mto huu wa Yordani, kwa njia ya nchi kavu. 23 Kwa sababu Bwana, Mungu wenu aliyakausha maji ya Yordani, mbele yenu, hata mlipokwisha kuvuka kama Bwana, Mungu wenu, alivyoitenda Bahari ya Shamu, aliyoikausha mbele yetu hata tulipokwisha kuvuka; 24 watu wote wa duniani wapate kujua mkono wa Bwana, ya kuwa ni mkono wenye uweza, ili wamche Bwana, Mungu wenu, milele.

Yoshua 5

1 Ikawa, wafalme wa Waamori, waliokaa ng'ambo ya Yordani pande za magharibi, na wafalme wote wa Wakanaani, waliokuwa karibu na bahari, waliposikia jinsi Bwana alivyoyakausha maji ya Yordani mbele ya wana wa Israeli, hata tulipokwisha kuvuka, basi mioyo yao iliyeyuka, wala haikuwamo roho ya nguvu ndani yao tena; kwa ajili ya wana wa Israeli. 2 Wakati huo Bwana akamwambia Yoshua, Haya, jifanyie visu vya mawe ya gumegume, watahiri tena wana wa Israeli mara ya pili. 3 Basi Yoshua akajifanyia visu vya mawe ya gumegume, akawatahiri wana wa Israeli huko Gibea-haaralothi. 4 Na sababu ya Yoshua kutahiri ni hii; watu wote waliotoka Misri, waliokuwa waume, hao watu waume wote waendao vitani walikufa katika bara njiani, baada ya wao kutoka Misri. 5 Kwa kuwa watu wote waliotoka walikuwa wamekwisha kutahiriwa; lakini watu wote waliozaliwa katika bara njiani walipokwisha kutoka Misri, hao hawakutahiriwa. 6 Kwa kuwa wana wa Israeli walitembea muda wa miaka arobaini barani, hata hilo taifa zima, yaani, watu waume waendao vitani, waliotoka Misri, walipokuwa wameangamia; kwa sababu hawakuisikiza sauti ya Bwana; nao ndio Bwana aliowaapia ya kwamba hatawaacha waione hiyo nchi, ambayo Bwana aliwaapia baba zao kwamba atatupa sisi; nchi ijaayo maziwa na asali. 7 Na watoto wao, aliowainua badala yao ndio hao aliowatahiri Yoshua; kwa kuwa wao walikuwa hawakutahiriwa, kwa maana walikuwa hawakuwatahiri njiani. 8 Ilikuwa walipokwisha kutahiriwa taifa zima, wakakaa kila mtu mahali pake maragoni, hata walipopoa. 9 Bwana akamwambia Yoshua, Siku hii ya leo nimeivingirisha hiyo aibu ya Misri iondoke juu yenu. Kwa hiyo jina la mahali pale likaitwa Gilgali, hata hivi leo. 10 Basi wana wa Israeli wakapanga hema zao huko Gilgali; nao wakala sikukuu ya pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi, jioni, katika nchi tambarare za Yeriko. 11 Nao wakala katika mazao ya nchi siku ya pili ya kuiandama hiyo sikukuu ya pasaka, mikate isiyotiwa chachu, na bisi, siku iyo hiyo. 12 Ndipo ile mana ikakoma siku ya pili yake, baada ya wao kuyala hayo mazao ya nchi; na hao wana wa Israeli hawakuwa na mana tena; lakini wakala katika viliwa vya nchi ya Kanaani mwaka huo. 13 Ikawa hapo Yoshua alipokuwa karibu na mji wa Yeriko, akavua macho yake na kuangalia, na tazama, mtu mume akasimama kumkabili mbele yake, naye alikuwa na upanga wazi mkononi mwake; Yoshua akamwendea, na kumwambia, Je! Wewe u upande wetu, au upande wa adui zetu? 14 Akasema, La, lakini nimekuja sasa, nili amiri wa jeshi la Bwana. Yoshua akapomoka kiusouso hata nchi, naye akasujudu, akamwuliza, Bwana wangu aniambia nini mimi mtumishi wake? 15 Huyo amiri wa jeshi la Bwana akamwambia Yoshua, Vua viatu vyako miguuni mwako; kwa kuwa mahali hapo usimamapo ni patakatifu. Yoshua akafanya vivyo.

Yoshua 6

1 Basi Yeriko ulikuwa umefungwa kabisa kwa sababu ya wana wa Israeli; hapana mtu aliyetoka wala hapana mtu aliyeingia. 2 Bwana akamwambia Yoshua, Tazama, nimeutia Yeriko katika mkono wako, na mfalme wake, na mashujaa wake. 3 Nanyi mtauzunguka mji huu, watu wote wa vita, mkiuzunguka mji mara moja. Fanya hivi siku sita. 4 Na makuhani saba watachukua tarumbeta saba za pembe za kondoo waume, mbele ya hilo sanduku; na siku ya saba mtauzunguka mji mara saba, nao makuhani watapiga tarumbeta zao. 5 Kisha itakuwa watakapopiga hizo pembe za kondoo waume kwa nguvu, nanyi mtakaposikia sauti ya tarumbeta, watu wote watapiga kelele kwa sauti kuu; na ukuta wa mji utaanguka chini pale pale, na hao watu watapanda, kila mtu akiendelea mbele kukabili. 6 Bali Yoshua, mwana wa Nuni, akawaita makuhani, akawaambia, Lichukueni sanduku la agano, tena makuhani saba na wachukue tarumbeta saba za pembe za kondoo waume mbele ya sanduku la Bwana. 7 Naye akawaambia watu, Piteni mbele, mkauzunguke mji, na hao watu wenye silaha na watangulie mbele ya sanduku la Bwana. 8 Basi ikawa Yoshua alipokwisha kusema na watu, wale makuhani saba, wenye kuzichukua tarumbeta saba za pembe za kondoo waume mbele za Bwana, wakatangulia, wakazipiga hizo tarumbeta; nalo sanduku la agano la Bwana likawafuata. 9 Wale watu wenye silaha walikwenda mbele ya hao makuhani waliozipiga tarumbeta, na wale waliokuwa nyuma wakalifuata hilo sanduku; makuhani wakizipiga tarumbeta walipokuwa wakienda. 10 Yoshua akawaamuru watu, akasema Msipige kelele, wala sauti zenu zisisikiwe, wala neno lo lote lisitoke kinywani mwenu, hata siku ile nitakapowaamuru kupiga kelele, ndipo mtakapopiga kelele. 11 Basi akalipeleka sanduku la Bwana liuzunguke huo mji, likauzunguka mara moja, kisha wakaenda kambini wakakaa kambini. 12 Yoshua akaondoka asubuhi na mapema, nao makuhani wakalichukua sanduku la Bwana. 13 Na wale makuhani saba wakazichukua tarumbeta saba za pembe za kondoo waume mbele ya sanduku la Bwana, wakaendelea wakazipiga tarumbeta; nao watu wenye silaha wakawatangulia, na hao waliokuwa nyuma wakalifuata sanduku la Bwana; makuhani wakizipiga tarumbeta walipokuwa wakienda. 14 Siku ya pili wakauzunguka mji mara moja, wakarejea kambini; ndivyo walivyofanya siku sita. 15 Ikawa siku ya saba wakaondoka asubuhi na mapema wakati wa mapambazuko, wakauzunguka mji vivyo hivyo mara saba; ila siku hiyo waliuzunguka huo mji mara saba. 16 Hata mara ya saba makuhani walipozipiga tarumbeta, Yoshua akawaambia watu, Pigeni kelele; kwa maana Bwana amewapeni mji huu. 17 Na mji huu utakuwa wakfu kwa Bwana, mji wenyewe na vitu vyote vilivyomo; isipokuwa Rahabu, yule kahaba, ataishi, yeye na watu wote walio pamoja naye nyumbani, kwa sababu aliwaficha hao wapelelezi tuliowatuma. 18 Na ninyi, msikose kujiepusha na kitu kilichowekwa wakfu; msije mkakitwaa kitu kilichowekwa wakfu, baada ya kukiweka wakfu; nanyi hivyo mtayafanya matuo ya Israeli kuwa yamelaaniwa na kuyafadhaisha. 19 Lakini fedha yote, na dhahabu, na vyombo vya shaba, na chuma, ni vitakatifu kwa Bwana; vitaletwa katika hazina ya Bwana. 20 Basi watu wakapiga kelele, na makuhani wakazipiga tarumbeta; hata ikawa, hapo watu waliposikia sauti ya tarumbeta hao watu wakapiga kelele kwa sauti kuu sana, na ule ukuta wa mji ukaanguka nchi kabisa, hata watu wakapanda juu, wakaingia katika mji, kila mtu akiendelea kukabili mbele; wakautwaa huo mji. 21 Basi wakaangamiza kabisa vitu vyote vilivyokuwa ndani ya mji, wanaume na wanawake, watoto na wazee, na ng'ombe, na kondoo, na punda, kwa makali ya upanga. 22 Naye Yoshua akawaambia wale wanaume wawili walioipeleleza nchi, Ingieni katika nyumba ya yule kahaba, mkamtoe huyo mwanamke mwenyewe na vitu vyote alivyo navyo, kama mlivyomwapia. 23 Basi wale vijana wapelelezi wakaingia, wakamtoa Rahabu, na baba yake, na mama yake, na ndugu zake, na vitu vyote walivyokuwa navyo, wakawatoa na jamaa zake wote pia; wakawaweka nje ya matuo ya Israeli. 24 Kisha wakauteketeza mji kwa moto, na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake; bali fedha, na dhahabu, na vyombo vya shaba, na vya chuma, wakavitia katika hazina ya nyumba ya Bwana. 25 Lakini Yoshua akamhifadhi Rahabu, yule kahaba, na watu wa nyumba ya baba yake, na vitu vyote alivyokuwa navyo; naye akakaa kati ya Israeli hata leo; kwa sababu aliwaficha wale wajumbe aliowatuma Yoshua ili kuupeleleza mji wa Yeriko. 26 Naye Yoshua akawaapisha kiapo wakati ule, akasema, Na alaaniwe mbele za Bwana mtu yule atakayeinuka na kuujenga tena mji huu wa Yeriko; ataweka msingi wake kwa kufiliwa na mzaliwa wa kwanza wake, tena atayasimamisha malango yake kwa kufiliwa na mtoto wake mwanamume aliye mdogo. 27 Basi Bwana alikuwa pamoja na Yoshua; sifa zake zikaenea katika nchi ile yote.

Yoshua 7

1 Lakini wana wa Israeli walifanya dhambi katika kitu kilichowekwa wakfu; maana Akani, mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila ya Yuda, alitwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; hasira ya Bwana ikawaka juu ya wana wa Israeli. 2 Kisha Yoshua akatuma watu kutoka Yeriko mpaka mji wa Ai, ulio karibu na Bethaveni, upande wa mashariki wa Betheli, akawaambia, akisema, Pandeni juu mkaipeleleze nchi, basi wakapanda juu wakaupeleleza Ai. 3 Wakarejea kwa Yoshua wakamwambia, Wasiende watu wote, ila waende watu kama elfu mbili, tatu, wakaupige Ai; usiwataabishe watu wote kwa kuwaendesha huko; maana watu hao ni wachache tu. 4 Basi watu wakaenda huko wapata elfu tatu tu; nao wakakimbia mbele ya watu wa Ai. 5 Watu wa Ai wakawapiga watu kama thelathini na sita; wakawafuatia kutoka mbele ya mlango mpaka Shebarimu, wakawapiga huko kwenye matelemko; mioyo ya watu ikayeyuka, ikawa kama maji. 6 Yoshua akararua mavazi yake, akaanguka kifudifudi mbele ya sanduku la Bwana hata jioni, yeye na wazee wa Israeli; wakatia mavumbi vichwani mwao. 7 Yoshua akasema, Ee Bwana MUNGU, kwa nini umewavusha watu hawa mto wa Yordani, ili kututia katika mikono ya Waamori, na kutuangamiza? Laiti tungelikuwa radhi kukaa ng'ambo ya Yordani 8 Ee Bwana, niseme nini baada ya Israeli kuwapa visogo adui zao? 9 Maana Wakanaani na wenyeji wote wa nchi hii watasikia habari hii, nao watatuzingira, na kulifuta jina letu katika nchi. Nawe utafanya nini kwa ajili ya jina lako kuu? 10 Bwana akamwambia Yoshua, Haya! Inuka, mbona umeanguka kifudifudi hivi? 11 Israeli wamefanya dhambi, naam, wamelivunja agano langu nililowaagiza; naam, wametwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; tena wameiba, tena wameficha na kuvitia pamoja na vitu vyao wenyewe. 12 Ndiposa wana wa Israeli hawawezi kusimama mbele ya adui zao; wakawapa visogo adui zao, kwa sababu wamelaaniwa; mimi sitakuwa pamoja nanyi tena, msipokiharibu kitu kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu. 13 Haya! Inuka, uwatakase watu, ukaseme, Jitakaseni, mwe tayari kesho; maana Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Kitu kilichowekwa wakfu kiko katikati yako, Ee Israeli; huwezi kusimama mbele ya adui zako, hata mtakapokiondoa kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu. 14 Basi asubuhi mtaletwa karibu nami kabila kwa kabila; kisha itakuwa ya kwamba kabila ile atakayoitwaa Bwana itakaribia jamaa kwa jamaa; na jamaa ile atakayoitwaa Bwana itakaribia nyumba kwa nyumba; na nyumba ile atakayoitwaa Bwana itakaribia mtu kwa mtu. 15 Tena itakuwa ya kwamba yeye atakayetwaliwa, naye anacho kitu kile kilichowekwa wakfu, atateketezwa kwa moto, yeye na vitu vyote alivyo navyo; kwa sababu amelivunja agano la Bwana, na kwa sababu ametenda upumbavu katika Israeli. 16 Basi Yoshua akaondoka asubuhi na mapema, akawasogeza Israeli kabila kwa kabila; kabila ya Yuda ikatwaliwa. 17 Akazisogeza jamaa za Yuda, akaitwaa jamaa ya Wazera; akaisogeza jamaa ya Wazera mtu kwa mtu; Zabdi akatwaliwa. 18 Akawasogeza watu wa nyumba yake mmoja mmoja; na Akani, mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila ya Yuda akatwaliwa. 19 Yoshua akamwambia Akani, Mwanangu, nakusihi, umtukuze Bwana, Mungu wa Israeli, ukaungame kwake; uniambie sasa ulilolitenda; usinifiche. 20 Akani akamjibu Yoshua, akasema, Kweli nimefanya dhambi juu ya Bwana, Mungu wa Israeli, nami nimefanya mambo haya na haya. 21 Nilipoona katika nyara joho nzuri ya Babeli, na shekeli mia mbili za fedha, na kabari ya dhahabu, uzani wake shekeli hamsini, basi nalivitamani nikavitwaa; tazama, vimefichwa mchangani katikati ya hema yangu, na ile fedha chini yake. 22 Basi Yoshua akatuma wajumbe wakapiga mbio mpaka hemani; na tazama, vile vitu vilikuwa vimefichwa hemani mwake, na ile fedha chini yake. 23 Wakavitoa kutoka hapo katikati ya hema, wakavileta kwa Yoshua, na kwa wana wa Israeli wote, nao wakaviweka chini mbele za Bwana. 24 Kisha Yoshua, na Israeli wote pamoja naye, wakamtwaa Akani, mwana wa Zera, na ile fedha, na Lile joho, na ile kabari ya dhahabu, na wanawe, na binti zake, na ng'ombe zake, na punda zake, na kondoo zake, na hema yake, na vitu vyote alivyokuwa navyo, wakavileta juu hata bonde la Akori. 25 Yoshua akasema, Mbona umetufadhaisha hivi? Bwana atakufadhaisha wewe leo. Ndipo Israeli wote wakampiga kwa mawe, kisha wakawateketeza kwa moto, na kuwapiga kwa mawe. 26 Kisha wakakusanya juu yake chungu kubwa ya mawe hata leo; naye Bwana akauacha ukali wa hasira yake. Kwa sababu hiyo jina la mahali pale likaitwa, Bonde la Akori, hata hivi leo.

Yoshua 8

1 Kisha Bwana akamwambia Yoshua, Usiche, wala usifadhaike; wachukue watu wote wa vita waende pamoja nawe, nanyi inukeni, mwende Ai, angalia, mimi nimemtia mkononi mwako huyo mfalme wa Ai, na watu wake, na mji wake, na nchi yake; 2 nawe utautenda mji wa Ai na mfalme wake kama ulivyoutenda mji wa Yeriko na mfalme wake; lakini nyara zake na wanyama wake wa mji mtavitwaa kuwa mateka yenu wenyewe; huo mji uuwekee waoteaji upande wa nyuma. 3 Basi Yoshua akainuka, na watu wote wa vita pamoja naye, ili waende Ai; Yoshua akachagua watu thelathini elfu, watu mashujaa wenye uwezo, akawapeleka wakati wa usiku. 4 Akawaagiza, akasema, Angalieni, mtaotea kuuvizia ule mji, upande wa nyuma wa mji; msiende mbali sana na mji, lakini kaeni tayari nyote; 5 na mimi, na watu wote walio pamoja nami, tutaukaribia mji; kisha itakuwa, hapo watakapotoka nje kupigana nasi, kama walivyofanya hapo kwanza, sisi tutakimbia mbele yao; 6 nao watatoka nje watufuate, hata tuwavute waende mbali na mji wao; kwa kuwa watasema, Wakimbia mbele yetu, kama walivyofanya kwanza; nasi tutakimbia mbele yao; 7 basi ninyi mtainuka mtoke hapo mwoteapo, na kuushika mji; kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, atautia mikononi mwenu. 8 Kisha itakuwa, mtakapoushika mji, ndipo mtauteketeza mji kwa moto; sawasawa na hilo neno la Bwana; angalieni, nimewaagiza. 9 Basi Yoshua akawatuma; nao wakaenda hata hapo watakapootea, wakakaa kati ya Betheli na Ai, upande wa magharibi wa Ai; lakini Yoshua akalala usiku huo kati ya watu. 10 Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akawakutanisha watu, kisha akatangulia kukwea kwenda Ai mbele ya hao watu, yeye na wazee wa Israeli. 11 Watu wote, hao wa vita, waliokuwa pamoja naye, wakaenda wakakaribia, na kufikilia mbele ya mji, wakatua upande wa kaskazini wa Ai; napo palikuwa na bonde kati ya yeye na Ai. 12 Kisha akatwaa watu kama elfu tano, akawaweka kuotea kati ya Betheli na Ai, upande wa magharibi wa huo mji. 13 Basi wakawaweka hao watu, jeshi zima lililokuwa upande wa kaskazini wa mji, na wale waliokuwa waotea upande wa magharibi wa mji; naye Yoshua akaenda usiku huo katikati ya hilo bonde. 14 Kisha ikawa hapo huyo mfalme wa Ai alipoona jambo hilo, ndipo walipofanya haraka, na wakaamka asubuhi na mapema, na watu waume wa mji wakatoka nje waende kupigana na Israeli, yeye na watu wake wote, kwa wakati ulioamriwa, kuikabili Araba; lakini hakujua ya kwamba walikuwako waviziao kinyume chake kwa upande wa nyuma wa mji. 15 Kisha Yoshua na watu wa Israeli wote walifanya kana kwamba wameshindwa mbele yao, wakakimbia kwa njia ya nyika. 16 Watu wote waliokuwa ndani ya mji waliitwa wakusanyike pamoja ili kuwafuatia; nao wakamfuatia Yoshua, wakasongea mbele na kuuacha mji. 17 Hakusalia mtu ye yote ndani ya Ai, au katika Betheli, asiyetoka nje kuwafuatia Israeli; wakauacha mji wazi na kuwafuatia Israeli. 18 Kisha Bwana akamwambia Yoshua, Haya, unyoshe huo mkuki ulio nao mkononi mwako, uuelekeze upande wa Ai; kwa kuwa nitautia mkononi mwako. Basi Yoshua akaunyosha huo mkuki uliokuwa mkononi mwake kuuelekea huo mji. 19 Wale watu waliovizia wakainuka kwa upesi kutoka mahali pao, nao wakapiga mbio mara hapo alipokuwa amekwisha unyosha mkono wake, wakaingia ndani ya mji, na kuushika; nao wakafanya haraka kuuteketeza kwa moto huo mji. 20 Kisha hapo hao watu wa Ai walipotazama nyuma yao, wakaona, na tazama, moshi wa huo mji ulikuwa unapaa juu kwenda mawinguni, nao hawakuwa na nguvu za kukimbia huku wala huku; na wale watu waliokuwa wamekimbia kuenenda nyikani wakageuka na kuwarudia hao waliokuwa wakiwafuatia. 21 Basi hapo Yoshua na Israeli wote walipoona ya kwamba hao waliovizia wamekwisha kuushika huo mji, na ya kwamba moshi wa mji umepaa juu, ndipo wakageuka tena, na kuwaua watu wa Ai. 22 Tena hao; wengine wakatoka nje kuutoka huo mji kinyume chao; basi hivyo walikuwa wa katikati ya Israeli, wengine upande huu na wengine upande huu; nao wakawapiga, hata wasimwache hata mmoja miongoni mwao aliyesalia, wala kupona. 23 Kisha wakamshika mfalme wa Ai ali hai, nao wakamleta kwa Yoshua. 24 Kisha ikawa, hapo Israeli walipokuwa wamekwisha kuwaua wenyeji wote wa Ai katika bara, hapo katika nyika walipokuwamo wakiwafuatia, nao walikuwa wamekwisha anguka wote kwa makali ya upanga, hata walipokuwa wameangamizwa wote, ndipo Israeli wakarejea Ai, na kuupiga huo mji kwa makali ya upanga. 25 Wote walioanguka siku hiyo waume kwa wake, walikuwa ni kumi na mbili elfu, yaani, watu wote wa mji wa Ai. 26 Kwani huyo Yoshua hakuuzuia mkono wake, huo ulionyosha huo mkuki, hata hapo alipokuwa amewaangamiza kabisa wenyeji wote wa Ai. 27 Isipokuwa wanyama wa mji na nyara za mji Israeli wakatwaa wenyewe kuwa ni mapato yao, sawasawa na hilo neno la Bwana alilomwamuru Yoshua. 28 Basi Yoshua akaupiga moto mji wa Ai, na kuufanya kuwa ni chungu ya magofu hata milele, kuwa ni ukiwa hata siku hii ya leo. 29 Na huyo mfalme wa Ai akamtundika katika mti hata wakati wa jioni; kisha hapo jua lilipokuchwa Yoshua akaagiza, nao wakauondoa mzoga wake katika huo mti, na kuutupa hapo penye maingilio ya lango la mji, kisha wakaweka pale juu yake chungu kubwa ya mawe, hata hivi leo. 30 Ndipo Yoshua alijenga madhabahu kwa Bwana, Mungu wa Israeli katika mlima Ebali. 31 Kama Musa, mtumishi wa Bwana, alivyowaamuru wana wa Israeli, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha torati ya Musa, madhabahu ya mawe yasiyochongwa, ambayo mtu hakutumia juu yake chombo cha chuma; nao wakatoa juu yake sadaka za kuteketezwa kwa Bwana, na kuchinja sadaka za amani. 32 Akaandika huko juu ya mawe hayo nakala ya torati ya Musa, aliyoiandika mbele ya wana wa Israeli. 33 Na Israeli wote, na wazee wao, na maakida yao, na makadhi yao, wakasimama upande huu wa sanduku na upande huu, mbele ya makuhani Walawi, waliolichukua sanduku la agano la Bwana, huyo aliyekuwa mgeni pamoja na huyo mzalia; nusu yao mbele ya mlima Gerizimu, na nusu yao mbele ya mlima Ebali, kama Musa, mtumishi wa Bwana, alivyoamuru, ili wawabarikie watu wa Israeli kwanza. 34 Na baadaye alisoma maneno yote ya torati, baraka na laana, sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati. 35 Hapakuwa na hata neno moja katika hayo aliyoamuru Musa, ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya kusanyiko lote la Israeli, na mbele ya wanawake, na watoto, na wageni waliokaa nao.

Yoshua 9

1 Kisha ikawa hapo wafalme wote waliokaa ng'ambo ya pili ya Yordani, hapo penye nchi ya vilima, na katika Shefela, na katika upande wa pwani yote ya bahari kubwa kuikabili Lebanoni, yaani, huyo Mhiti, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, waliposikia habari ya mambo hayo; 2 ndipo walipojikutanisha pamoja wenyewe kwa wenyewe, ili kupigana na Yoshua, na hao Israeli, kwa nia moja. 3 Lakini wenyeji wa Gibeoni waliposikia habari ya hayo yote Yoshua aliyokuwa amewatenda watu wa Yeriko, na wa Ai, 4 wao wakatenda kwa hila, nao wakaenda na kujifanya kama ndio wajumbe, wakaenda na magunia makuukuu juu ya punda zao, na viriba vya mvinyo vilivyokuwa vikuukuu vilivyoraruka-raruka, na kutiwa viraka; 5 na viatu vilivyotoboka na kushonwa-shonwa katika miguu yao, na mavao makuukuu waliyokuwa wanavaa; tena mkate wote wa chakula chao ulikuwa umekauka na kuingia koga. 6 Nao wakamwendea Yoshua hata maragoni huko Gilgali, nao wakamwambia yeye na watu wa Israeli, Sisi tumetoka nchi ya mbali sana; basi kwa hiyo fanyeni agano pamoja nasi. 7 Basi watu wa Israeli wakawaambia hao Wahivi, Labda mwakaa kati yetu; nasi tutawezaje kufanya agano nanyi? 8 Nao wakamwambia Yoshua, Sisi tu watumishi wako. Yoshua akawauliza, Ninyi ni nani? Nanyi mwatoka wapi? 9 Nao wakamwambia, Sisi watumishi wako twatoka nchi iliyo mbali sana, kwa sababu ya jina la Bwana, Mungu wako; kwa kuwa sisi tumesikia sifa zake, na habari ya hayo yote aliyofanya huko Misri, 10 na habari ya hayo yote aliyowatenda wale wafalme wawili wa Waamori, waliokuwa huko ng'ambo ya pili ya Yordani, maana huyo Sihoni, mfalme wa Heshboni, na Ogu, mfalme wa Bashani, aliyekuwa huko Ashtarothi. 11 Kisha wazee wetu, na wenyeji wote wa nchi yetu, walinena nasi na kutuambia, Chukueni vyakula mkononi mwenu kwa ajili ya safari, mwende mkawalaki watu hao, na kuwaambia, Sisi tu watumishi wenu; basi sasa fanyeni agano nasi. 12 Huu mkate wetu tuliutwaa ukali moto katika nyumba zetu, siku hiyo tuliyotoka kuja kwenu, uwe chakula chetu; lakini sasa, tazama, umekauka, na kuingia koga; 13 na viriba vyetu hivi, tulivyovitia divai, vilikuwa ni vipya; sasa, tazama, vimeraruka-raruka; na haya mavazi yetu na viatu vyetu vimekuwa vikuukuu kwa vile tulivyokuja safari ya mbali sana. 14 Basi hao watu wakatwaa katika vyakula vyao, wala wasitake shauri kinywani mwa Bwana. 15 Naye Yoshua akafanya amani pamoja nao, na kufanya agano nao, ili kwamba waachwe hai; na wakuu wa mkutano wakawaapia. 16 Kisha ikawa, mwisho wa siku ya tatu baada ya kufanya hilo agano nao, walisikia habari ya kuwa watu hao ni jirani zao, na ya kwamba waliketi kati yao. 17 Kisha wana wa Israeli walisafiri, wakaifikilia miji ya watu hao siku ya tatu. Basi miji ya watu hao ilikuwa ni hii, Gibeoni, na Kefira, na Beerothi, na Kiriath-yearimu. 18 Wana wa Israeli hawakuwapiga, kwa sababu wakuu wa mkutano walikuwa wamekwisha kuwaapia kwa Bwana, Mungu wa Israeli. Nao mkutano wote wakawanung'unikia hao wakuu. 19 Lakini wakuu wote waliwaambia mkutano wote, Sisi tumewaapia kwa Bwana, Mungu wa Israeli; basi sasa hatuwezi kuwagusa watu hawa. 20 Tutawafanyia neno hili, kisha tutawaacha wawe hai; hasira isije juu yetu, kwa ajili ya hicho kiapo tulichowaapia. 21 Wakuu waliwaambia, Waacheni wawe hai; basi wakawa wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya mkutano wote; vile vile kama hao wakuu walivyowaambia. 22 Basi Yoshua akawaita, akanena nao, na kuwaambia, Mbona ninyi mmetudanganya, huku mkisema, Sisi tu mbali sana na ninyi; nanyi kumbe! Mwakaa kati yetu? 23 Basi sasa mmelaaniwa kisha hatakosekana kuwapo mtu wa kwenu aliye mtumwa, wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu. 24 Nao wakamjibu Yoshua, na kusema, Ni kwa sababu ya sisi watumishi wako kuambiwa hakika, jinsi huyo Bwana, Mungu wako alivyomwamuru mtumishi wake Musa kuwapa ninyi nchi hii yote, na kuwaangamiza wenyeji wote wa nchi hii watoke mbele zenu; kwa sababu hii tuliogopa mno kwa ajili ya uhai wetu kwa sababu yenu, nasi tumefanya neno hili. 25 Basi sasa, tazama, sisi tu mkononi mwako; basi kama uonavyo kuwa ni vyema na haki kwako wewe kututenda, tutende vivyo. 26 Naye akawafanyia hivyo, na kuwaokoa na mkono wa wana wa Israeli, ili wasiwaue. 27 Siku iyo hiyo Yoshua akawafanya kuwa ni wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya mkutano, na kwa ajili ya madhabahu ya Bwana, hata siku hii ya leo, katika mahali hapo atakapopachagua.

Yoshua 10

1 Basi ikawa hapo Adoni-sedeki, mfalme wa Yerusalemu, aliposikia jinsi Yoshua alivyoushika mji wa Ai na kuuharibu kabisa; kama alivyoufanyia mji wa Yeriko na mfalme wake, akaufanya vivyo Ai na mfalme wake; na jinsi wenyeji waliokaa Gibeoni walivyofanya amani na Israeli, na ya kwamba walikuwa kati yao; 2 ndipo wakacha mno, kwa sababu Gibeoni ulikuwa ni mji mkubwa, kama ilivyo miji ya kifalme mmojawapo, tena kwa sababu ulikuwa ni mji mkubwa kupita Ai, tena watu wake wote walikuwa ni mashujaa. 3 Basi kwa hiyo Adoni-sedeki, mfalme wa Yerusalemu, akatuma ujumbe kwa Hohamu, mfalme wa Hebroni, na kwa Piramu, mfalme wa Yarmuthi, na kwa Yafia, mfalme wa Lakishi, na kwa Debiri, mfalme wa Egloni, akiwaambia, 4 Haya, kweeni mje kwangu, mnisaidie, tuupige Gibeoni; kwa sababu umefanya mapatano ya amani pamoja na Yoshua na wana wa Israeli. 5 Ndipo hao wafalme watano wa Waamori, mfalme wa Yerusalemu, na mfalme wa Hebroni na mfalme wa Yarmuthi na mfalme wa Lakishi, na mfalme wa Egloni, wakakutana pamoja, kisha wakakwea, wao na jeshi zao zote, na kupanga marago yao kinyume cha Gibeoni, na kuupiga vita. 6 Ndipo watu wa Gibeoni wakatuma wajumbe kwenda kwa Yoshua huko Gilgali maragoni, wakamwambia, Usiulegeze mkono wako hata ukatuacha sisi watumishi wako; uje kwetu kwa upesi, utuokoe, na kutusaidia; kwa sababu wafalme wote wa Waamori wakaao katika nchi ya vilima wamekutana pamoja juu yetu. 7 Basi Yoshua akakwea kutoka Gilgali, yeye, na watu wa vita wote pamoja naye, na mashujaa wenye uwezo pia wote. 8 Bwana akamwambia Yoshua, Usiwache watu hao; kwa kuwa mimi nimekwisha kuwatia mikononi mwako; hapana mtu awaye yote miongoni mwao atakayesimama mbele yako. 9 Basi Yoshua akawafikilia ghafula; kwani alikwea kutoka Gilgali kwenda usiku kucha. 10 Bwana naye akawatapanya mbele ya Israeli, naye Israeli akawaua uuaji ulio mkuu hapo Gibeoni, akawafukuza waikimbilie hiyo njia ya kukwelea kwenda Beth-horoni, na kuwapiga hata kufikilia Azeka, tena hata kufikilia Makeda. 11 Kisha ikawa, hapo walipokuwa wakimbia mbele ya Israeli, hapo walipokuwa katika kutelemkia Beth-horoni, ndipo Bwana alipowatupia mawe makubwa kutoka mbinguni juu yao hata kufikilia Azeka, nao wakafa; hao waliokufa kwa kuuawa na hayo mawe ya barafu walikuwa ni wengi kuliko hao waliouawa na wana wa Israeli kwa upanga. 12 Ndipo Yoshua akanena na Bwana katika siku hiyo ambayo Bwana aliwatoa Waamori mbele ya wana wa Israeli; akasema mbele ya macho ya Israeli, Wewe Jua, simama kimya juu ya Gibeoni; Na wewe Mwezi, simama katika bonde la Aiyaloni. 13 Ndipo jua likasimama, na mwezi ukatulia, Hata hilo taifa lilipokuwa limekwisha jipatiliza juu ya adui zao. 14 Haikuwapo siku nyingine mfano wa siku hiyo katika siku zilizotangulia mbele yake wala katika hizo zilizoandama baada yake, hata ikawa yeye Bwana kuisikia sauti ya binadamu; kwa kuwa Bwana alipiga vita kwa ajili ya Israeli. 15 Basi Yoshua akarudi, na Israeli wote wakarudi pamoja naye, mpaka maragoni hapo Gilgali. 16 Na hawa wafalme watano wakakimbia, wakajificha ndani ya pango la Makeda. 17 Kisha Yoshua aliambiwa habari hiyo, ya kwamba, Hao wafalme watano wameonekana, nao wa hali ya kujificha ndani ya pango la Makeda 18 Basi Yoshua akasema, Haya, vingirisheni mawe makubwa mdomoni mwa lile pango, kisha wekeni watu hapo ili kuwalinda; 19 lakini msikae ninyi; wafuatieni adui zenu, mwapige hao walio nyuma; msiwaache wakaingia ndani ya miji yao; kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, amewatia mikononi mwenu. 20 Kisha ikawa, hapo Yoshua, na wana wa Israeli, walipokuwa wamekwisha kuwaua watu wengi mno, hata wakaangamizwa, na hayo mabaki yao yaliyowasalia walipokuwa wamekwisha ingia katika miji yao yenye boma, 21 ndipo hao watu wote wakamrudia Yoshua maragoni huko Makeda salama; hakuna mtu awaye yote aliyetoa ulimi kinyume cha hao wana wa Israeli hata mmojawapo. 22 Kisha Yoshua akasema, Haya, funua mdomo wa pango, mniletee hao wafalme watano hapa nje ya pango. 23 Nao wakafanya, wakamletea hao wafalme watano hapo nje ya pango, yaani, mfalme wa Yerusalemu, na mfalme wa Hebroni, na mfalme wa Yarmuthi, na mfalme wa Lakishi, na mfalme wa Egloni. 24 Kisha ikawa hapo walipomletea Yoshua hao wafalme watano hapo nje, Yoshua akawaita wanaume wote wa Israeli, akawaambia majemadari wa watu wa vita waliokwenda naye, Haya, jongeeni karibu, mweke nyayo za miguu yenu katika shingo za wafalme hawa. Nao wakajongea karibu, wakatia nyayo zao katika shingo zao. 25 Yoshua akawaambia, Msiche, wala msifadhaike; iweni hodari na wa mioyo ya ushujaa; kwa kuwa ndivyo Bwana atakavyowafanyia adui zenu wote ambao mwapigana nao. 26 Baadaye Yoshua akawapiga, na kuwaua, akawatundika katika miti mitano; nao wakawa wakitundikwa katika hiyo miti hata jioni. 27 Kisha wakati wa kuchwa jua, Yoshua akatoa amri, nao wakawatelemsha katika hiyo miti, na kuwatupa katika lile pango ambamo walikuwa walijificha kisha wakatia mawe makubwa mdomoni mwa pango, hata hivi leo. 28 Siku hiyo Yoshua akautwaa mji wa Makeda, akaupiga kwa makali ya upanga, na mfalme wake; akawaangamiza kabisa na wote pia waliokuwamo ndani yake, hakumwacha hata mmoja aliyesalia; naye akamfanyia huyo mfalme wa Makeda kama alivyomfanyia huyo mfalme wa Yeriko. 29 Kisha Yoshua akapita kutoka hapo Makeda, mpaka Libna, na Israeli wote pamoja naye, nao wakapiga Libna; 30 Bwana akautia na mji huo pia pamoja na mfalme wake mkononi mwa Israeli; naye akaupiga kwa makali ya upanga, na wote pia waliokuwamo ndani yake; hakumwacha hata mmoja aliyesalia ndani yake; naye akamtenda mfalme wake kama alivyomtenda huyo mfalme wa Yeriko. 31 Kisha Yoshua akapita kutoka hapo Libna, na Israeli wote pamoja naye, wakafika Lakishi, wakapanga marago mbele yake na kupigana nao; 32 Bwana akautia huo mji wa Lakishi mkononi mwa Israeli, naye akautwaa siku ya pili, akaupiga kwa makali ya upanga, na wote pia waliokuwamo ndani yake, sawasawa na hayo yote aliyoutenda Libna. 33 Wakati huo Horamu, mfalme wa Gezeri, akakwea ili kuusaidia Lakishi, lakini Yoshua akampiga yeye na watu wake, hata asimsazie hata mtu mmoja. 34 Kisha Yoshua akapita kutoka hapo Lakishi, na Israeli wote pamoja naye, hata wakafikilia Egloni; nao wakapanga marago mbele yake, na kupigana nao; 35 siku iyo hiyo wakautwaa, nao wakaupiga kwa makali ya upanga, na wote pia waliokuwamo ndani yake akawaangamiza kabisa siku hiyo, sawasawa na hayo yote aliyoufanyia mji wa Lakishi. 36 Kisha Yoshua akakwea kutoka hapo Egloni, na Israeli wote pamoja naye, hata wakafikilia Hebroni; nao wakapigana nao; 37 wakautwaa, na kuupiga kwa makali ya upanga, na mfalme wake, na miji yake yote, na wote waliokuwamo ndani yake; hakumwacha aliyesalia hata mtu mmoja, sawasawa na hayo yote aliyoufanyia huo mji wa Egloni; lakini akauangamiza kabisa, na wote pia waliokuwamo ndani yake. 38 Kisha Yoshua akarudi, na Israeli wote pamoja naye, hata Debiri; nao wakapigana nao; 39 kisha akautwaa, na mfalme wake, na miji yake yote; nao wakawapiga kwa makali ya upanga, wakawaangamiza kabisa wote pia waliokuwamo ndani yake; hakumwacha hata mmoja aliyesalia; kama alivyoufanyia Hebroni aliufanyia na Debiri vivyo, na mfalme wake; kama alivyoufanyia Libna, na mfalme wake. 40 Basi Yoshua akaipiga nchi hiyo yote, nchi ya vilima, na nchi ya Negebu, na nchi ya Shefela, na nchi ya matelemko, na wafalme wake wote; hakumwacha aliyesalia hata mmoja; lakini akawaharibu kabisa wote waliokuwa wavuta pumzi, kama Bwana, Mungu wa Israeli, alivyoamuru. 41 Yoshua akawapiga kutoka Kadesh-barnea mpaka Gaza, na nchi yote ya Gosheni, hata Gibeoni. 42 Na wafalme hao wote na nchi zao Yoshua akatwaa, wakati huo, kwa sababu yeye Bwana, Mungu wa Israeli, alipigana kwa ajili ya Israeli, 43 Kisha Yoshua akarudi, na Israeli wote pamoja naye, hata marago yao huko Gilgali.

Yoshua 11

1 Kisha ikawa, hapo huyo Yabini, mfalme wa Hazori, aliposikia habari ya mambo hayo, akatuma mjumbe aende kwa Yobabu, mfalme wa Madoni, na kwa mfalme wa Shimroni, na mfalme wa Akshafu, 2 na hao wafalme waliokuwa upande wa kaskazini, katika nchi ya vilima, na katika Araba upande wa kusini wa Kinerethi, na katika Shefela, na katika nchi zilizoinuka za Dori upande wa magharibi, 3 na kwa Mkanaani upande wa mashariki, na upande wa magharibi, na kwa Mwamori, na Mhiti, na Mperizi na Myebusi katika nchi ya vilima, na kwa Mhivi pale chini ya Hermoni katika nchi ya Mispa. 4 Nao wakatoka nje, wao na jeshi zao zote pamoja nao, watu wengi mno, kama mchanga ulio ufuoni mwa bahari kwa wingi, pamoja na farasi na magari mengi sana. 5 Wafalme hao wote wakakutana pamoja; wakaenda na kupanga mahema yao pamoja hapo penye maji ya Meromu, ili kupigana na Israeli. 6 Bwana akamwambia Yoshua, Usiche wewe kwa ajili ya hao; kwani kesho wakati kama huu nitawatoa hali wameuawa wote mbele ya Israeli; utawatema farasi zao, na magari yao utayapiga moto. 7 Basi Yoshua akaenda, na watu wote wa vita pamoja naye, ili kupigana nao hapo penye maji ya Meromu ghafula; wakawaangukia. 8 Bwana akawatia mkononi mwa Israeli, nao wakawapiga, na kuwafukuza hata kufikilia Sidoni ulio mkuu, na hata kufikilia Misrefoth-maimu, tena hata kufikilia bonde la Mispa upande wa mashariki; wakawapiga hata wasiwasaze hata mtu mmoja aliyesalia. 9 Yoshua akawafanyia vile vile kama Bwana alivyomwamuru; akawatema farasi zao, na magari yao akayapiga moto. 10 Yoshua akarudi wakati huo na kuutwaa Hazori, akampiga mfalme wa Hazori kwa upanga; kwa kuwa Hazori hapo kwanza ulikuwa ni kichwa cha falme hizo zote. 11 Nao wakawapiga wote pia waliokuwamo ndani ya Hazori kwa makali ya upanga, wakawaangamiza kabisa; hakusazwa hata mmoja aliyevuta pumzi; kisha akauteketeza Hazori kwa moto. 12 Tena miji yote ya wafalme hao, na wafalme wake wote, Yoshua akawatwaa, akawapiga kwa makali ya upanga, na kuwaangamiza kabisa; vile vile kama huyo Musa mtumishi wa Bwana alivyomwamuru. 13 Lakini katika habari ya miji hiyo iliyosimama katika vilima vyao, Israeli hawakuipiga moto miji hiyo, isipokuwa ni mji wa Hazori tu; mji huo Yoshua aliupiga moto. 14 Tena nyara zote za miji hiyo, na wanyama wa miji, wana wa Israeli walitwaa kuwa nyara zao wenyewe; lakini kila mtu wakampiga kwa makali ya upanga, hata walipokuwa wamewaangamiza wote, wala hawakumsaza mmoja mwenye kuvuta pumzi. 15 Vile vile kama Bwana alivyomwamuru Musa mtumishi wake, ndivyo Musa alivyomwamuru Yoshua; naye Yoshua akafanya vivyo; hakukosa kufanya neno lo lote katika hayo yote Bwana aliyomwamuru Musa. 16 Hivyo Yoshua akatwaa nchi hiyo yote, hiyo nchi ya vilima, na nchi yote ya Negebu, na nchi yote ya Gosheni, na hiyo Shefela, na hiyo Araba na nchi ya vilima vilima ya Israeli, na hiyo nchi tambarare; 17 tangu kilima cha Halaki, kiendeleacho upande wa Seiri, mpaka Baal-gadi katika bonde la Lebanoni chini ya kilima cha Hermoni; naye akawatwaa wafalme wao wote, akawapiga, na kuwaua. 18 Yoshua akapiga vita siku nyingi na wafalme hao wote. 19 Haukuwapo mji hata mmoja uliofanya amani na wana wa Israeli, isipokuwa ni wale Wahivi wenye kukaa Gibeoni; wakaitwaa yote vitani. 20 Kwa kuwa lilikuwa ni la Bwana kuifanya mioyo yao kuwa migumu, hata wakatoka kupigana na Israeli, ili apate kuwaangamiza kabisa, wasihurumiwe lakini apate kuwaangamiza, kama vile Bwana alivyomwamuru Musa. 21 Wakati huo Yoshua akaenda na kuwakatilia mbali hao Waanaki watoke nchi ya vilima, kutoka Hebroni, na kutoka Debiri, na kutoka Anabu, na kutoka katika nchi yote ya vilima vilima ya Yuda, na kutoka katika nchi yote ya vilima vilima ya Israeli; Yoshua akawaangamiza kabisa na miji yao. 22 Hawakusalia Waanaki hata mmoja katika nchi ya wana wa Israeli; isipokuwa katika Gaza, na katika Gathi, na katika Ashdodi walisalia. 23 Basi Yoshua akaitwaa hiyo nchi yote, sawasawa na hayo yote Bwana aliyokuwa amemwambia Musa; Yoshua naye akawapa Israeli kuwa ni urithi wao, sawasawa na walivyogawanyikana kwa kabila zao. Kisha nchi ikatulia isiwe na vita tena.

Yoshua 12

1 Basi hawa ndio wafalme wa nchi, ambao wana wa Israeli waliwapiga na kuimiliki nchi yao ng'ambo ya pili ya Yordani, upande wa maawio ya jua, kutoka bonde la Amoni mpaka mlima wa Hermoni, na nchi yote ya Araba upande wa mashariki; 2 Sihoni mfalme wa Waamori, aliyekaa huko Heshboni, naye ndiye aliyetawala toka Aroeri, ulioko kando ya bonde la Arnoni, na toka huo mji ulio katikati ya bonde, na nusu ya Gileadi, hata kuufikilia mto wa Yaboki, mpaka wa hao wana wa Amoni; 3 na nchi ya Araba mpaka bahari ya Kinerethi, kuelekea mashariki, tena mpaka bahari ya Ataba, mpaka Bahari ya Chumvi, kwendea mashariki, njia ya kwendea Beth-yeshimothi; tena upande wa kusini, chini ya matelemko ya Pisga; 4 tena mpaka wa Ogu mfalme wa Bashani, aliyekuwa wa hayo mabaki ya hao Warefai, aliyekaa Ashtarothi na Edrei, 5 naye alitawala katika mlima wa Hermoni, na katika Saleka, na katika Bashani yote, hata mpaka wa Wageshuri, na Wamaaka, na nusu ya Gileadi, mpaka wa huyo Sihoni mfalme wa Heshboni. 6 Musa mtumishi wa Bwana na wana wa Israeli wakawapiga; naye Musa mtumishi wa Bwana akawapa Wareubeni, na Wagadi, na nusu ya kabila ya Manase iwe urithi wao. 7 Hawa ni wafalme wa hiyo nchi ambao Yoshua na wana wa Israeli waliwapiga ng'ambo ya pili ya Yordani upande wa magharibi, kutoka Baal-gadi katika bonde la Lebanoni mpaka kilima cha Halaki, kilichoelekea Seiri; Yoshua naye akawapa kabila za Israeli iwe milki yao sawasawa na magawanyo yao; 8 katika nchi ya vilima, na katika Shefela, na katika nchi ya Araba, na katika matelemko, na katika bara, na katika Negebu; nchi ya Mhiti, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi; 9 mfalme wa Yeriko, mmoja; mfalme wa Ai, ulio karibu na Betheli, mmoja; 10 mfalme wa Yerusalemu, mmoja; mfalme wa Hebroni, mmoja; 11 mfalme wa Yarmuthi, mmoja; na mfalme wa Lakishi, mmoja; 12 mfalme wa Egloni, mmoja; na mfalme wa Gezeri, mmoja; 13 mfalme wa Debiri, mmoja; na mfalme wa Gederi, mmoja; 14 mfalme wa Horma, mmoja; na mfalme wa Aradi, mmoja; 15 mfalme wa Libna, mmoja; na mfalme wa Adulamu, mmoja; 16 mfalme wa Makeda, mmoja; na mfalme wa Betheli, mmoja; 17 mfalme wa Tapua, mmoja; na mfalme wa Heferi, mmoja; 18 mfalme wa Afeka, mmoja; na mfalme wa Lasharoni, mmoja; 19 mfalme wa Madoni, mmoja; na mfalme wa Hazori, mmoja; 20 mfalme wa Shimron-meroni, mmoja; na mfalme wa Akshafu, mmoja; 21 mfalme wa Taanaki, mmoja; na mfalme wa Megido, mmoja; 22 na mfalme wa Kedeshi, mmoja; mfalme wa Yokneamu wa Karmeli, mmoja; 23 mfalme wa Dori katika kilima cha Dori, mmoja; na mfalme wa makabila katika Gilgali, mmoja; 24 na mfalme wa Tirsa, mmoja; wafalme hao wote walikuwa ni thelathini na mmoja.

Yoshua 13

1 Basi Yoshua alipokuwa mzee, na kwendelea sana miaka yake, Bwana akamwambia, Wewe umekuwa mzee na kwendelea sana miaka yako, kisha inasalia nchi nyingi sana bado kumilikiwa. 2 Nchi iliyosalia ni hii; nchi zote za Wafilisti, na Wageshuri wote; 3 kutoka Shihori, hicho kijito kilichokabili Misri, hata mpaka wa Ekroni upande wa kaskazini, nchi inayohesabiwa kuwa ni ya hao Wakanaani; mashehe matano wa hao Wafilisti; Wagaza, na Waashdodi, na Waashkeloni, na Wagiti, na Waekroni; tena Waavi, 4 upande wa kusini; nchi yote ya Wakanaani na Meara iliyo ya Wasidoni, mpaka Afeka, hata mpaka wa Waamori; 5 na nchi ya Wagebali na Lebanoni yote, upande wa kuelekea maawio ya jua, kutoka Baal-gadi ulio chini ya mlima wa Hermoni mpaka kufikilia maingilio ya Hamathi; 6 na watu wote wenye kuikaa nchi ya vilima kutoka Lebanoni hata Misrefoth-maimu, maana, hao Wasidoni wote; hao wote nitawafukuza watoke mbele ya wana wa Israeli; lakini wewe uwape Israeli kuwa ni urithi wao, kama nilivyokuamuru. 7 Basi sasa gawanya nchi hii, iwe urithi wa hizi kabila kenda, na nusu ya kabila ya Manase. 8 Pamoja na yeye, Wareubeni na Wagadi walipata urithi wao, waliopewa na Musa, huko ng'ambo ya Yordani upande wa mashariki, vile vile kama huyo Musa mtumishi wa Bwana alivyowapa; 9 kutoka huko Aroeri, iliyo pale ukingoni mwa bonde la Amoni, na huo mji ulio pale katikati ya bonde, na nchi tambarare yote ya Medeba mpaka Diboni; 10 na miji yote ya Sihoni mfalme wa Waamori, aliyetawala katika Heshboni, hata mpaka wa wana wa Amoni; 11 na Gileadi na mpaka wa Wageshuri, na Wamaaka, na mlima wa Hermoni wote, na Bashani yote mpaka Saleka; 12 ufalme wote wa Ogu uliokuwa katika Bashani, huyo aliyekuwa akitawala katika Ashtarothi na katika Edrei (huyo alisalia katika mabaki ya wale Warefai); kwa kuwa Musa aliwapiga hao na kuwafukuza. 13 Pamoja na hayo wana wa Israeli hawakuwafukuza Wageshuri, wala Wamaaka; lakini Wageshuri na Wamaaka wamekaa kati ya Israeli, hata siku hii ya leo. 14 Lakini hakuwapa watu wa kabila ya Lawi urithi uwao wote; maana sadaka za Bwana, Mungu wa Israeli, zisongezwazo kwa njia ya moto ndizo urithi wake huyo, kama alivyomwambia. 15 Musa akawapa kabila ya wana wa Reubeni kwa kadiri ya jamaa zao. 16 Mpaka wao ulikuwa kutoka hapo Aroeri, iliyo pale ukingoni mwa bonde la Arnoni, na huo mji ulio katikati ya bonde, na nchi tambarare yote iliyo karibu na Medeba; 17 na Heshboni na miji yake yote iliyoko katika bonde; na Diboni, na Bamoth-baali, na Beth-baal-meoni; 18 na Yahasa, na Kedemothi, na Mefaathi; 19 na Kiriathaimu, na Sibma, na Sereth-shahari katika kilima cha hilo bonde; 20 na Beth-peori, na nchi za matelemko ya Pisga, na Beth-yeshimothi; 21 na miji yote ya nchi tambarare, na ufalme wote wa Sihoni mfalme wa Waamori, aliyekuwa akitawala katika Heshboni, aliyepigwa na Musa pamoja na hao wakubwa wa Midiani, nao ni Evi, na Rekemu, na Suri, na Huri, na Reba, hao mashehe wa Sihoni, waliokuwa katika nchi hiyo. 22 Balaamu naye, huyo mwana wa Beori, huyo mchawi, wana wa Israeli walimwua kwa upanga kati ya hao wengine waliowaua. 23 Na mpaka wa wana wa Reubeni ulikuwa ni mto wa Yordani, na mpaka wake. Huo ndio urithi wa wana wa Reubeni sawasawa na jamaa zao, miji yake na vijiji vyake. 24 Musa akawapa kabila ya Gadi, hao wana wa Gadi, kwa kadiri ya jamaa zao. 25 Mpaka wao ulikuwa ni Yazeri, na miji hiyo ya Gileadi, na nusu ya nchi ya wana wa Amoni, mpaka Aroeri uliokabili Raba; 26 tena kutoka Heshboni mpaka Ramath-Mizpe, na Betonimu; tena kutoka Mahanaimu hata mpaka wa Debiri; 27 tena katika bonde, Beth-haramu, na Bethnimira, na Sukothi, na Safoni, hiyo iliyosalia ya ufalme wa Sihoni mfalme wa Heshboni, yaani mto wa Yordani na mpaka wake, mpaka mwisho wa bahari ya Kinerethi ng'ambo ya pili ya Yordani upande wa mashariki. 28 Huo ndio urithi wa wana wa Gadi sawasawa na jamaa zao, miji yake na vijiji vyake. 29 Kisha Musa akawapa hao wa nusu ya kabila ya Manase urithi wao; ulikuwa ni wa hiyo nusu ya kabila ya wana wa Manase sawasawa na jamaa zao. 30 Na mpaka wao ulikuwa kutoka huko Mahanaimu, Bashani yote, na ufalme wote wa Ogu mfalme wa Bashani, na miji yote ya Yairi, iliyo katika Bashani, miji sitini; 31 na nusu ya Gileadi, na Ashtarothi, na Edrei, hiyo miji ya ufalme wa Ogu katika Bashani, ilikuwa ni ya wana wa Makiri mwana wa Manase maana, kwa hiyo nusu ya wana wa Makiri sawasawa na jamaa zao. 32 Hizi ndizo mirathi ambazo Musa alizigawanya katika nchi tambarare za Moabu, ng'ambo ya pili ya Yordani, kukabili Yeriko, upande wa mashariki. 33 Lakini Musa hakuwapa kabila ya Lawi urithi uwao wote; yeye Bwana, Mungu wa Israeli, ndiye urithi wao, kama alivyowaambia.

Yoshua 14

1 Kisha hizi ndizo nchi ambazo wana wa Israeli walizitwaa katika nchi ya Kanaani, ambazo Eleazari kuhani, na Yoshua mwana wa Nuni, na vichwa vya nyumba za mababa wa kabila za Israeli, waliwagawanyia, 2 kwa kuandama hiyo kura ya urithi wao, vile vile kama Bwana alivyoamuru kwa mkono wa Musa, kwa ajili ya hizo kabila kenda, na hiyo nusu ya kabila. 3 Kwa kuwa Musa alikuwa amekwisha kuwapa urithi hizo kabila mbili na nusu, ng'ambo ya pili ya Yordani; lakini hakuwapa Walawi urithi uwao wote kati yao. 4 Kwa kuwa wana wa Yusufu walikuwa kabila mbili, Manase na Efraimu; nao hawakuwapa Walawi sehemu katika hiyo nchi, isipokuwa waliwapa miji wapate kuikaa, pamoja na viunga vyake kwa ajili ya wanyama wao wa mifugo, na kwa ajili ya riziki zao. 5 Vile vile kama Bwana alivyomwamuru Musa, hao wana wa Israeli walifanya vivyo, nao wakaigawanya hiyo nchi. 6 Wakati huo wana wa Yuda walimkaribia Yoshua hapo Gilgali; na Kalebu, mwana wa Yefune, huyo Mkenizi, akamwambia, Wewe wajua hilo neno Bwana alilomwambia Musa, huyo mtu wa Mungu, katika habari zangu, na katika habari zako wewe, tulipokuwa katika Kadesh-barnea. 7 Mimi nilikuwa mtu wa miaka arobaini umri wangu, hapo Musa mtumishi wa Bwana aliponituma niende kutoka Kadesh-barnea ili kuipeleleza hiyo nchi; nami nilimletea habari tena, kama ilivyokuwa ndani ya moyo wangu. 8 Lakini wale ndugu zangu waliokwea kwenda pamoja nami waliiyeyusha mioyo ya watu; ila mimi nilimfuata Bwana, Mungu wangu, kwa utimilifu. 9 Kisha Musa akaniapia siku hiyo, akasema, Hakika hiyo nchi ambayo miguu yako imekanyaga itakuwa ni urithi kwako wewe, na kwa watoto wako milele, kwa sababu wewe umemfuata Bwana, Mungu wako, kwa utimilifu. 10 Sasa basi, angalia, yeye Bwana ameniweka hai, kama alivyosema, miaka hii arobaini na mitano, tangu wakati huo Bwana alipomwambia Musa neno hilo, wakati Israeli waliokuwa wakienenda barani; na sasa tazama, hivi leo nimepata miaka themanini na mitano umri wangu. 11 Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani. 12 Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena. 13 Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake. 14 Kwa hiyo Hebroni ukawa urithi wa Kalebu, mwana wa Yefune, Mkenizi, hata leo; kwa sababu alimwandama Bwana, Mungu wa Israeli, kwa utimilifu. 15 Basi jina la Hebroni hapo kwanza uliitwa Kiriath-arba; huyo Arba alikuwa ni mtu mkubwa kupita wenziwe wote katika hao Waanaki. Hiyo nchi nayo ikatulia, vita vikakoma.

Yoshua 15

1 Kura ya kabila ya wana wa Yuda kwa kuandama jamaa zao ilikuwa kufikilia hata mpaka wa Edomu, hata bara ya Sini upande wa kusini, huko mwisho upande wa kusini. 2 Mpaka wao wa kusini ulikuwa kutoka mwisho wa Bahari ya Chumvi, kutoka ile hori ielekeayo kusini; 3 nao ukaendelea upande wa kusini wa kukwea kwenda Akrabimu, kisha ukaendelea hata Sini, kisha ukaenda upande wa kusini wa Kadesh-barnea, kisha ukaendelea karibu na Hesroni, kisha ukafikilia Adari, na kuzunguka kwendea Karka; 4 kisha ukaendelea hata Azmoni, na kutokea hapo penye kijito cha Misri; na matokeo ya huo mpaka yalikuwa baharini; huu ndio mpaka wenu wa upande wa kusini. 5 Na mpaka wa upande wa mashariki ulikuwa Bahari ya Chumvi, hata mwisho wa mto wa Yordani. Na mpaka wa upande wa kaskazini ulikuwa kutoka pale penye hori ya baharini mwisho wa mto wa Yordani; 6 na huo mpaka ukaendelea hata Beth-hogla, kisha ukaendelea upande wa kaskazini wa Beth-araba; kisha mpaka ukaendelea hata jiwe la Bohani mwana wa Reubeni; 7 kisha mpaka ukaendelea hata Debiri kutoka bonde la Akori, vivyo ukaendelea upande wa kaskazini, kwa kuelekea Gilgali, iliyo mkabala wa kukwelea kwenda Adumimu, ulio upande wa kusini wa mto; kisha huo mpaka ukaendelea hata ukafikilia maji ya Enshemeshi, na matokeo yake yalikuwa hapo Enrogeli; 8 kisha mpaka ukaendelea karibu na bonde la mwana wa Hinomu, na kufikilia ubavuni mwa huyu Myebusi upande wa kusini (ndio Yerusalemu); kisha mpaka ukaendelea hata kilele cha mlima ulio pale mkabala wa bonde la Hinomu upande wa magharibi, lililo pale mwisho wa bonde la Warefai upande wa kaskazini; 9 kisha mpaka ulipigwa kutoka juu ya mlima huo hata kufikilia chemchemi ya maji ya Neftoa kisha ukatokea hata miji ya kilima cha Efroni; kisha mpaka ulipigwa hata kufikilia Baala (ndio Kiriath-yearimu); 10 kisha mpaka ukazunguka kutoka Baala kwendelea upande wa magharibi hata kilima Seiri, kisha ukaendelea hata upande wa mlima wa Yearimu upande wa kaskazini (huo ndio Kesaloni), kisha ukatelemkia Beth-shemeshi, na kwendelea karibu na Timna; 11 kisha mpaka ukatokea hata kufikilia upande wa Ekroni upande wa kaskazini; tena mpaka ulipigwa hata Shikroni, na kwendelea hata kilima cha Baala, kisha ukatokea hapo Yabneeli; na matokeo ya mpaka yalikuwa baharini. 12 Na mpaka wa upande wa magharibi ulifikilia hata bahari kubwa, na mpaka wake. Huo ndio mpaka wa wana wa Yuda kwa kuzunguka kote kote sawasawa na jamaa zao. 13 Kisha alimpa huyo Kalebu mwana wa Yefune sehemu kati ya wana wa Yuda, kama Bwana alivyomwamuru Yoshua, maana ni Kiriath-arba, ni huyo Arba aliyekuwa babaye Anaki (huo ndio Hebroni). 14 Huyo Kalebu aliwafukuza watoke hapo hao wana watatu wa Anaki, nao ni Sheshai, na Ahimani, na Talmai, wana wa Anaki. 15 Kisha akakwea kutoka huko ili kuwaendea wenyeji wa Debiri; jina la Debiri hapo kwanza lilikuwa Kiriath-seferi. 16 Kalebu akasema, Yeye atakayeupiga Kiriath-seferi na kuutwaa, mimi nitampa Aksa binti yangu awe mkewe. 17 Naye Othnieli mwana wa Kenazi, nduguye Kalebu, aliutwaa; basi akampa Aksa binti yake awe mkewe. 18 Kisha ikawa, hapo huyo mwanamke alipokwenda kwa mumewe, akamtaka aombe shamba kwa baba yake; akashuka katika punda wake; Kalebu akamwuliza, Wataka nini? 19 Huyo mwanamke akasema, Nipe baraka; kwa kuwa umeniweka katika nchi ya kusini, unipe na chemchemi za maji pia. Ndipo akampa chemchemi za maji ya juu, na chemchemi za maji ya chini. 20 Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Yuda sawasawa na jamaa zao. 21 Miji ya mwisho ya kabila ya wana wa Yuda upande wa kuelekea mpaka wa Edomu katika nchi ya Negebu ilikuwa ni Kabseeli, na Ederi, na Yaguri; 22 na Kina, na Dimona, na Adada; 23 na Kedeshi, na Hazori, na Ithnani; 24 na Zifu, na Telemu, na Bealothi; 25 na Hazor-hadata, na Kerioth-hezroni (ndio Hazori); 26 na Amamu, na Shema, na Molada; 27 na Hasar-gada, na Heshmoni, na Bethpeleti; 28 na Hasarshuali, na Beer-sheba, na Biziothia; 29 na Baala, na Iyimu, na Esemu; 30 na Eltoladi, na Kesili, na Horma; 31 na Siklagi, na Madmana, na Sansana; 32 na Lebaothi, na Shilhimu, na Aini, na Rimoni; miji hiyo yote ni miji ishirini na kenda, pamoja na vijiji vyake. 33 Katika nchi ya Shefela, Eshtaoli, na Sora, na Ashna, 34 na Zanoa, na Enganimu, na Tapua, na Enamu; 35 na Yarmuthi, na Adulamu, na Soko, na Azeka; 36 na Shaarimu, na Adithaimu, na Gedera, na Gederothaimu miji kumi na minne, pamoja na vijiji vyake. 37 Senani, na Hadasha, na Migdal-gadi; 38 na Dilani, na Mispe, na Yoktheeli; 39 na Lakishi, na Boskathi, na Egloni; 40 na Kaboni, na Lamasi, na Kithilishi; 41 na Gederothi, na Beth-dagoni, na Naama, na Makeda; miji kumi na sita, pamoja na vijiji vyake. 42 Libna, na Etheri, na Ashani; 43 na Yifta, na Ashna, na Nesibu; 44 na Keila, na Akizibu, na Maresha; miji kenda, pamoja na vijiji vyake. 45 Ekroni, pamoja na miji yake na vijiji vyake; 46 kutoka huko Ekroni mpaka baharini, yote iliyokuwa upande wa Ashdodi, pamoja na vijiji vyake. 47 Ashdodi, na miji yake na vijiji vyake; na Gaza, na miji yake na vijiji vyake; mpaka kijito cha Misri, na bahari kubwa, na mpaka wake. 48 Na katika nchi ya vilima, Shamiri, na Yatiri, na Soko; 49 na Dana, na Kiriath-sana (ambao ni Debiri); 50 na Anabu, na Eshtemoa, na Animu; 51 na Gosheni, na Holoni, na Gilo; miji kumi na mmoja, pamoja na vijiji vyake. 52 Arabu, na Duma, na Eshani; 53 na Yanumu, na Beth-tapua, na Afeka; 54 na Humta, na Kiriath-arba (ndio Hebroni), na Siori; miji kenda, pamoja na vijiji vyake. 55 Maoni, na Karmeli, na Zifu, na Yuta; 56 na Yezreeli, na Yokdeamu, na Zanoa; 57 na Kaini, na Gibea, na Timna; miji kumi, pamoja na vijiji vyake. 58 Halhuli, na Bethsuri, na Gedori; 59 na Maarathi, na Bethanothi, Eltekoni; miji sita, pamoja na vijiji vyake. 60 Kiriath-baali (ndio Kiriath-yearimu), na Raba; miji miwili, pamoja vijiji vyake. 61 Huko nyikani, Betharaba, na Midini, na Sekaka; 62 na Nibshani, na huo Mji wa Chumvi, na Engedi; miji sita, pamoja na vijiji vyake. 63 Tena katika habari ya Wayebusi, hao wenye kukaa Yerusalemu, wana wa Yuda hawakuweza kuwatoa; lakini hao Wayebusi walikaa pamoja na wana wa Yuda huko Yerusalemu hata hivi leo.

Yoshua 16

1 Kura ya wana wa Yusufu ilianza kutoka mto wa Yordani hapo Yeriko, hapo penye maji ya Yeriko upande wa mashariki, maana, ni hiyo nyika, kukwea kutoka Yeriko kati ya hiyo nchi ya vilima mpaka Betheli; 2 kisha ikatoka huko Betheli kwendelea Luzu, kisha ikaendelea hata kuufikilia mpaka wa Waarki mpaka Atarothi; 3 kisha ikatelemkia upande wa magharibi hata kuufikilia mpaka wa Wayafleti, hata mpaka wa Beth-horoni ya chini, hata kufikilia Gezeri; na matokeo yake yalikuwa hapo baharini. 4 Na wana wa Yusufu, Manase na Efraimu, walitwaa urithi wao. 5 Na mpaka wa wana wa Efraimu kwa kuandama jamaa zao ulikuwa hivi; mpaka na urithi wao upande wa mashariki ulikuwa ni Ataroth-adari, hata Beth-horoni wa juu; 6 kisha mpaka ukatokea kwendelea upande wa magharibi huko Mikmeta upande wa kaskazini; kisha mpaka ukazunguka kwendea upande wa mashariki hata Taanath-shilo, kisha ukaendelea upande wa mashariki wa Yanoa; 7 kisha ulitelemka kutoka Yanoa hata Atarothi, na Naara, kisha ukafikilia Yeriko, na kutokea hapo penye mto wa Yordani. 8 Kutoka hapo Tapua mpaka ukaendelea upande wa magharibi hata kijito cha Kana; na matokeo yake yalikuwa baharini. Huo ndio urithi wa hao wana wa Efraimu kwa kuandama jamaa zao; 9 pamoja na ile miji iliyotengwa kwa ajili ya wana wa Efraimu katikati ya urithi wa hao wana wa Manase, miji yote pamoja na vijiji vyake. 10 Nao hawakuwatoa Wakanaani waliokuwa Wakikaa Gezeri; lakini hao Wakanaani waliketi kati ya Efraimu, hata hivi leo, wakawa watumishi wa kufanya kazi za shokoa.

Yoshua 17

1 Kisha hii ndiyo kura iliyoiangukia kabila ya Manase; maana, yeye alikuwa ni mzaliwa wa kwanza, wa Yusufu. Katika habari za Makiri, mzaliwa wa kwanza wa Manase, babaye Gileadi, kwa sababu alikuwa mtu wa vita, basi alikuwa na Gileadi na Bashani. 2 Na kura ilikuwa ni ya hao wana wa Manase waliosalia kwa kuandama jamaa zao; kwa wana wa Abiezeri, na kwa wana wa Heleki, na kwa wana wa Asrieli, na kwa wana wa Shekemu, na kwa wana wa Heferi, na kwa wana wa Shemida; hao ndio wana waume wa Manase, mwana wa Yusufu, kwa kuandama jamaa zao. 3 Lakini Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na wana waume ila binti; na majina ya hao binti zake walikuwa wakiitwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. 4 Nao wakakaribia mbele ya Eleazari, kuhani, na mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, na mbele ya mashehe, wakasema, Bwana alimwamuru Musa kutupa sisi urithi kati ya ndugu zetu; basi kwa kuiandama hiyo amri ya Bwana akawapa urithi kati ya ndugu za baba yao. 5 Kisha kura zilizomwangukia Manase zilikuwa ni sehemu kumi, mbali na nchi ya Gileadi na Bashani, iliyo ng'ambo ya Yordani; 6 kwa sababu hao binti za Manase walikuwa na urithi katika wanawe waume; na nchi ya Gileadi ilikuwa ni mali ya hao wana waume wa Manase waliosalia. 7 Mpaka wa Manase ulikuwa kutoka Asheri hata Mikmeta, ulioelekea Shekemu; tena mpaka ukaendelea upande wa kuume, hata kuwafikilia wenyeji wa Entapua. 8 Hiyo nchi ya Tapua ilikuwa ni mali ya Manase; lakini ule mji wa Tapua uliokuwa katika mpaka wa Manase ulikuwa ni mali ya wana wa Efraimu. 9 Tena mpaka ulitelemkia mpaka kijito cha Kana, upande wa kusini wa hicho kijito; miji hiyo ilikuwa ya Efraimu kati ya miji ya Manase; na mpaka wa Manase ulikuwa upande wa kaskazini wa hicho kijito, na matokeo yake yalikuwa baharini; 10 upande wa kusini ilikuwa ni mali ya Efraimu, na upande wa kaskazini ilikuwa ni mali ya Manase, na bahari ilikuwa mpaka wake; nao wakafikilia hata Asheri upande wa kaskazini, na kufikilia hata Isakari upande wa mashariki. 11 Tena Manase alikuwa na miji katika Isakari na katika Asheri, nayo ni hii, Bethsheani na vijiji vyake, na Ibleamu na miji yake, na wenyeji wa Dori na miji yake, na wenyeji wa Endori na miji yake, na wenyeji wa Taanaki na miji yake, na wenyeji wa Megido na miji yake, hata mahali patatu palipoinuka. 12 Lakini wana wa Manase hawakuweza kuwafukuza wenyeji wa miji hiyo; bali hao Wakanaani walijikaza ili wakae katika nchi hiyo. 13 Kisha ikawa, hapo hao wana wa Israeli walipokuwa wamepata nguvu zaidi, ndipo wakawatenza nguvu hao Wakanaani wafanye kazi ya shokoa, wala hawakuwafukuza kabisa. 14 Kisha wana wa Yusufu wakanena na Yoshua, wakasema, Kwa nini umenipa mimi kura moja tu na fungu moja kuwa ni urithi wangu, kwa kuwa mimi ni taifa kubwa la watu, kwa sababu Bwana amenibarikia hata hivi sasa? 15 Yoshua akawaambia, Kwamba wewe u taifa kubwa la watu, haya, kwea uende mwituni, ujikatie mahali hapo kwa ajili ya nafsi yako katika nchi ya Waperizi, na ya hao Warefai; ikiwa hiyo nchi ya vilima ya Efraimu ni nyembamba, haikutoshi. 16 Wana wa Yusufu wakasema, Hiyo nchi ya vilima haitutoshi sisi; lakini Wakanaani wote wakaao katika nchi ya bondeni wana magari ya chuma, hao walio katika Bethsheani na miji yake, na hao walio katika bonde la Yezreeli pia. 17 Kisha Yoshua alinena na nyumba ya Yusufu, maana, ni Efraimu na Manase, akawaambia, Wewe u taifa kubwa la watu, nawe una uwezo mwingi; hutapata kura moja tu; 18 lakini hiyo nchi ya vilima itakuwa ni yako; maana, ijapokuwa ni mwitu, wewe utaukata, na matokeo yake yatakuwa ni yako; kwa kuwa wewe utawafukuza hao Wakanaani, wajapokuwa wana magari ya chuma, wajapokuwa ni wenye uwezo.

Yoshua 18

1 Kisha mkutano mzima wa wana wa Israeli walikutana pamoja hapo Shilo, wakasimamisha hema ya kukutania kuko; nayo nchi ilikuwa imeshindwa mbele zao. 2 Zilisalia katika wana wa Israeli kabila saba ambazo hazijagawanyiwa bado urithi wao. 3 Yoshua akawauliza wana wa Israeli, akasema, Je! Hata lini mtakuwa walegevu katika kuingia kwenu na kuimiliki hiyo nchi, ambayo yeye Bwana, Mungu wa baba zenu, amewapa? 4 Haya, jichagulieni watu watatu kwa ajili ya kila kabila; nami nitawatuma, nao watainuka waende kati ya hiyo nchi, na kuiandika kama urithi wao ulivyo; kisha watanijilia mimi. 5 Watu hao wataigawanya nchi iwe mafungu saba; Yuda atakaa katika mpaka wake huko upande wa kusini, na nyumba ya Yusufu watakaa katika mpaka wao upande wa kaskazini. 6 Nanyi mtaiandika nchi iwe mafungu saba, kisha hayo maandiko yake mtaniletea mimi hapa; nami nitawapigia kura hapa mbele ya Bwana, Mungu wetu. 7 Kwa maana Walawi hawana fungu kati yenu; Kwa kuwa huo ukuhani wa Bwana ndio urithi wao; tena Gadi, na Reubeni, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, wamekwisha pata urithi wao ng'ambo ya pili ya Yordani upande wa mashariki, ambao walipewa na Musa, mtumishi wa Bwana. 8 Basi watu hao wakainuka wakaenda; kisha Yoshua aliwaagiza wale waliokwenda kuiandika nchi, akawaambia, Endeni, mkapite katikati ya nchi, na kuiandika habari zake, kisha mnijie tena hapa, nami nitawapigia kura kwa ajili yenu hapo mbele za Bwana huko Shilo. 9 Basi watu hao wakaenda, wakapita katikati ya nchi, wakaandika habari zake katika chuo, na kuigawanya kwa miji yake, hata iwe mafungu saba, kisha wakamrejea Yoshua maragoni huko Shilo. 10 Kisha Yoshua akapiga kura kwa ajili yao hapo mbele za Bwana katika Shilo; huko Yoshua akawagawanyia wana wa Israeli hiyo nchi sawasawa na mafungu yao. 11 Kisha ilizuka kura ya kabila ya wana wa Benyamini kwa kuandama jamaa zao; na mpaka wa hiyo kura yao ukatokea kati ya wana wa Yuda na wana wa Yusufu. 12 Mpaka wao upande wa kaskazini ulikuwa kutoka mto wa Yordani; kisha mpaka ukaendelea kufikilia ubavuni mwa mji wa Yeriko upande wa kaskazini, kisha ukaendelea kati ya nchi ya vilima kwa kuelekea upande wa magharibi; na matokeo yake yalikuwa hapo penye nyika ya Bethaveni. 13 Kisha mpaka ukaendelea kutoka hapo na kufikilia mji wa Luzu, ubavuni mwa Luzu (ndio Betheli), kwa upande wa kusini; kisha mpaka ukatelemkia Ataroth-adari, karibu na mlima ulio upande wa kusini wa Beth-horoni wa chini. 14 Kisha mpaka uliendelea na kuzunguka upande wa magharibi wa kuelekea kusini, kutoka huo mlima ulio mkabala wa Beth-horoni upande wa kusini; na matokeo yake yalikuwa hapo Kiriath-baali (ndio Kiriath-yearimu), ni mji wa wana wa Yuda; huo ndio upande wa magharibi. 15 Na upande wa kusini ulikuwa ukitoka upande wa mwisho wa Kiriath-yearimu, na mpaka ukatokea upande wa magharibi, ukaendelea hata chemchemi ya maji, pale Neftoa; 16 kisha mpaka ulitelemka hata mwisho wa mlima ulio pale mkabala wa bonde la mwana wa Hinomu, lililo pale katika bonde la Warefai, upande wa kaskazini; nao ukatelemkia mpaka bonde la Hinomu, hata ubavuni mwa Myebusi upande wa kusini, kisha ukatelemka hata Enrogeli, 17 kisha ulipigwa upande wa kaskazini, nao ukatokea hapo Enshemeshi, ukatokea hata kufikilia Gelilothi, ambao ni mkabala wa makweleo ya Adumimu; kisha ulitelemka hata jiwe la Bohani mwana wa Reubeni; 18 kisha ukaendelea mbele ubavuni kuikabili Araba, upande wa kuelekea kaskazini, nao ukatelemka hata hiyo Araba; 19 kisha mpaka ukaendelea mbele ubavuni mwa Beth-hogla upande wa kaskazini; na matokeo ya mpaka yalikuwa katika ile hori ya kaskazini ya Bahari ya Chumvi, mwisho wa kusini wa mto wa Yordani; huo ndio mpaka wa upande wa kusini. 20 Na mto wa Yordani ulikuwa ndio mpaka wake upande wa mashariki. Huo ndio urithi wa wana wa Benyamini, kwa kuandama mipaka yake kwa kuuzunguka kote kote, sawasawa na jamaa zao. 21 Basi miji ya kabila ya wana wa Benyamini kwa kuandama jamaa zao ilikuwa ni Yeriko, na Beth-hogla, na Emek-kesisi, 22 na Bethiaraba, na Semaraimu, na Betheli; 23 na Avimu, na Para, na Ofra; 24 na Kefar-amoni, na Ofni, na Geba; miji kumi na miwili, pamoja na vijiji vyake; 25 na Gibeoni, na Rama, na Beerothi; 26 na Mispa, na Kefira, na Moza; 27 na Rekemu, na Irpeeli, na Tarala; 28 na Zela, na Elefu, na huyo Myebusi (ndio Yerusalemu), na Gibeathi, na Kiriathi; miji kumi na minne, pamoja na vijiji vyake. Huo ndio urithi wa wana wa Benyamini kwa kuandama jamaa zao. Yoshua, Chapter 1Kisha mkutano mzima wa wana wa Israeli walikutana pamoja hapo Shilo, wakasimamisha hema ya kukutania kuko; nayo nchi ilikuwa imeshindwa mbele zao. 2 Zilisalia katika wana wa Israeli kabila saba ambazo hazijagawanyiwa bado urithi wao. 3 Yoshua akawauliza wana wa Israeli, akasema, Je! Hata lini mtakuwa walegevu katika kuingia kwenu na kuimiliki hiyo nchi, ambayo yeye Bwana, Mungu wa baba zenu, amewapa? 4 Haya, jichagulieni watu watatu kwa ajili ya kila kabila; nami nitawatuma, nao watainuka waende kati ya hiyo nchi, na kuiandika kama urithi wao ulivyo; kisha watanijilia mimi. 5 Watu hao wataigawanya nchi iwe mafungu saba; Yuda atakaa katika mpaka wake huko upande wa kusini, na nyumba ya Yusufu watakaa katika mpaka wao upande wa kaskazini. 6 Nanyi mtaiandika nchi iwe mafungu saba, kisha hayo maandiko yake mtaniletea mimi hapa; nami nitawapigia kura hapa mbele ya Bwana, Mungu wetu. 7 Kwa maana Walawi hawana fungu kati yenu; Kwa kuwa huo ukuhani wa Bwana ndio urithi wao; tena Gadi, na Reubeni, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, wamekwisha pata urithi wao ng'ambo ya pili ya Yordani upande wa mashariki, ambao walipewa na Musa, mtumishi wa Bwana. 8 Basi watu hao wakainuka wakaenda; kisha Yoshua aliwaagiza wale waliokwenda kuiandika nchi, akawaambia, Endeni, mkapite katikati ya nchi, na kuiandika habari zake, kisha mnijie tena hapa, nami nitawapigia kura kwa ajili yenu hapo mbele za Bwana huko Shilo. 9 Basi watu hao wakaenda, wakapita katikati ya nchi, wakaandika habari zake katika chuo, na kuigawanya kwa miji yake, hata iwe mafungu saba, kisha wakamrejea Yoshua maragoni huko Shilo. 10 Kisha Yoshua akapiga kura kwa ajili yao hapo mbele za Bwana katika Shilo; huko Yoshua akawagawanyia wana wa Israeli hiyo nchi sawasawa na mafungu yao. 11 Kisha ilizuka kura ya kabila ya wana wa Benyamini kwa kuandama jamaa zao; na mpaka wa hiyo kura yao ukatokea kati ya wana wa Yuda na wana wa Yusufu. 12 Mpaka wao upande wa kaskazini ulikuwa kutoka mto wa Yordani; kisha mpaka ukaendelea kufikilia ubavuni mwa mji wa Yeriko upande wa kaskazini, kisha ukaendelea kati ya nchi ya vilima kwa kuelekea upande wa magharibi; na matokeo yake yalikuwa hapo penye nyika ya Bethaveni. 13 Kisha mpaka ukaendelea kutoka hapo na kufikilia mji wa Luzu, ubavuni mwa Luzu (ndio Betheli), kwa upande wa kusini; kisha mpaka ukatelemkia Ataroth-adari, karibu na mlima ulio upande wa kusini wa Beth-horoni wa chini. 14 Kisha mpaka uliendelea na kuzunguka upande wa magharibi wa kuelekea kusini, kutoka huo mlima ulio mkabala wa Beth-horoni upande wa kusini; na matokeo yake yalikuwa hapo Kiriath-baali (ndio Kiriath-yearimu), ni mji wa wana wa Yuda; huo ndio upande wa magharibi. 15 Na upande wa kusini ulikuwa ukitoka upande wa mwisho wa Kiriath-yearimu, na mpaka ukatokea upande wa magharibi, ukaendelea hata chemchemi ya maji, pale Neftoa; 16 kisha mpaka ulitelemka hata mwisho wa mlima ulio pale mkabala wa bonde la mwana wa Hinomu, lililo pale katika bonde la Warefai, upande wa kaskazini; nao ukatelemkia mpaka bonde la Hinomu, hata ubavuni mwa Myebusi upande wa kusini, kisha ukatelemka hata Enrogeli, 17 kisha ulipigwa upande wa kaskazini, nao ukatokea hapo Enshemeshi, ukatokea hata kufikilia Gelilothi, ambao ni mkabala wa makweleo ya Adumimu; kisha ulitelemka hata jiwe la Bohani mwana wa Reubeni; 18 kisha ukaendelea mbele ubavuni kuikabili Araba, upande wa kuelekea kaskazini, nao ukatelemka hata hiyo Araba; 19 kisha mpaka ukaendelea mbele ubavuni mwa Beth-hogla upande wa kaskazini; na matokeo ya mpaka yalikuwa katika ile hori ya kaskazini ya Bahari ya Chumvi, mwisho wa kusini wa mto wa Yordani; huo ndio mpaka wa upande wa kusini. 20 Na mto wa Yordani ulikuwa ndio mpaka wake upande wa mashariki. Huo ndio urithi wa wana wa Benyamini, kwa kuandama mipaka yake kwa kuuzunguka kote kote, sawasawa na jamaa zao. 21 Basi miji ya kabila ya wana wa Benyamini kwa kuandama jamaa zao ilikuwa ni Yeriko, na Beth-hogla, na Emek-kesisi, 22 na Bethiaraba, na Semaraimu, na Betheli; 23 na Avimu, na Para, na Ofra; 24 na Kefar-amoni, na Ofni, na Geba; miji kumi na miwili, pamoja na vijiji vyake; 25 na Gibeoni, na Rama, na Beerothi; 26 na Mispa, na Kefira, na Moza; 27 na Rekemu, na Irpeeli, na Tarala; 28 na Zela, na Elefu, na huyo Myebusi (ndio Yerusalemu), na Gibeathi, na Kiriathi; miji kumi na minne, pamoja na vijiji vyake. Huo ndio urithi wa wana wa Benyamini kwa kuandama jamaa zao.

Yoshua 19

1 Kisha kura ya pili ilitokea kwa ajili ya Simeoni, maana, kwa ajili ya hiyo kabila ya wana wa Simeoni, kwa kuandama jamaa zao; na urithi wao ulikuwa katikati ya urithi wa wana wa Yuda. 2 Miji waliyokuwa nayo katika urithi wao ni Beer-sheba, na Sheba, na Molada; 3 na Hasarshuali, na Bala, na Esemu; 4 na Eltoladi, na Bethuli, na Horma; 5 na Siklagi, na Bethmarkabothi, na Hasarsusa; 6 na Bethlebaothi, na Sharuheni; miji kumi na mitatu, pamoja na vijiji vyake; 7 na Aini, na Rimoni, na Etheri, na Ashani; miji minne, pamoja na vijiji vyake; 8 tena vijiji vyote vilivyozunguka miji hiyo kote kote mpaka Baalath-beeri, Rama wa Kusini. Huo ndio urithi wa kabila ya wana wa Simeoni kwa kuandama jamaa zao. 9 Huo urithi wa hao wana wa Simeoni ulitoka katika fungu la wana wa Yuda; kwa maana hilo fungu la wana wa Yuda lilikuwa ni kubwa mno kwao; kwa hiyo wana wa Simeoni walikuwa na urithi katikati ya urithi wao. 10 Kisha kura ya tatu ilitokea kwa ajili ya wana wa Zabuloni kwa kuandama jamaa zao; na mpaka wa urithi wao ulifikilia hata Saridi; 11 kisha mpaka wao ukakwea kwendelea upande wa magharibi, hata kufikilia Marala, nao ukafikilia hata Dabeshethi; nao ukafikilia kijito cha maji kilicho mkabala wa Yokneamu; 12 kisha ukazunguka kutoka Saridi kwendelea upande wa mashariki kwa kuelekea maawio ya jua hata kufikilia mpaka wa Kisiloth-ubori; kisha ukatokea hata Daberathi, kisha ukakwea kwendelea Yafia; 13 kutoka hapo ukaendelea kuelekea mashariki mpaka Gath-heferi, hata kufikilia Ethkasini; kisha ukatokea huko Rimoni ufikiliao hata Nea; 14 kisha mpaka uliizunguka nchi hiyo kwa upande wa kaskazini hata Hanathoni; kisha matokeo yake yalikuwa katika bonde la Iftaeli; 15 na Katathi, na Nahalali, na Shimroni, na Idala, na Bethlehemu; miji kumi na miwili, pamoja na vijiji vyake. 16 Huu ndio urithi wa wana wa Zabuloni kwa kuandama jamaa zao; miji hii pamoja na vijiji vyake. 17 Kisha kura ya nne ilitokea kwa ajili ya Isakari, maana, ni kwa ajili ya wana wa Isakari kwa kuandama jamaa zao. 18 Na mpaka wao ulifikilia Yezreeli, na Kesulothi, na Shunemu; 19 na Hafaraimu, na Shioni, na Anaharathi; 20 na Rabithu, na Kishioni, na Ebesi; 21 na Remethi, na Enganimu, na Enhada, na Bethpasesi; 22 na mpaka ukafikilia hata Tabori, na Shahasuma na Bethshemeshi; na matokeo ya mpaka wao yalikuwa katika mto wa Yordani; miji kumi na sita, pamoja na vijiji vyake. 23 Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Isakari kwa kuandama jamaa zao; miji hiyo pamoja na vijiji vyake. 24 Kisha kura ya tano ilitokea kwa ajili ya kabila ya wana wa Asheri kwa kuandama jamaa zao. 25 Na mpaka wao ulikuwa ni Helkathi, na Hali, na Beteni, na Akishafu; 26 na Alameleki, na Amadi, na Mishali; nao ukafikilia hata Karmeli upande wa magharibi, tena ulifikilia hata Shihor-libnathi; 27 kisha ukazunguka kuelekea maawio ya jua mpaka Beth-dagoni, nao ukafikilia hata Zabuloni, tena mpaka bonde la Iftaeli upande wa kaskazini hata Bethemeki na Neyeli; kisha ukatokea hata Kabuli upande wa kushoto; 28 na Ebroni, na Rehobu, na Hamoni, na Kana, hata kufikilia Sidoni mkuu; 29 kisha mpaka ulizunguka kuelekea Rama, na mji wa Tiro ulio na boma; kisha mpaka ulizunguka kuelekea Hosa; na matokeo yake yalikuwa baharini katika nchi ya Akzibu; 30 na Uma pia, na Afeka, na Rehobu; miji ishirini na miwili, pamoja na vijiji vyake. 31 Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Asheri kwa kuandama jamaa zao; miji hii pamoja na vijiji vyake. 32 Kisha kura ya sita ikatokea kwa ajili ya wana wa Naftali, maana, ni kwa ajili ya wana wa Naftali kwa kuandama jamaa zao. 33 Na mpaka wao ulikuwa kutoka Helefu, tokea ule mwaloni ulio katika Saananimu, na Adami-nekebu, na Yabineeli, hata kufikilia Lakumu; na matokeo yake yalikuwa katika mto wa Yordani; 34 tena mpaka ulizunguka kwendelea upande wa magharibi hata Aznoth-tabori, tena kutoka hapo ukaendelea mpaka Hukoki; kisha ukafikilia hata Zabuloni upande wa kusini, tena ulifikilia hata Asheri upande wa magharibi, tena ulifikilia hata Yuda hapo katika mto wa Yordani kwa upande wa kuelekea maawio ya jua. 35 Na miji yenye boma ilikuwa ni hii, Sidimu, na Seri, na Hamathi, na Rakathi, na Kinerethi; 36 na Adama, na Rama, na Hazori; 37 na Kedeshi, na Edrei, na Enhasori; 38 na Ironi, na Migdal-eli, na Horemu, na Bethanathi, na Bethshemeshi; miji kumi na kenda, pamoja na vijiji vyake. 39 Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Naftali kwa kuandama jamaa zao; miji hiyo pamoja na vijiji vyake. 40 Kisha kura ya saba ilitokea kwa ajili ya kabila ya wana wa Dani kwa kuandama jamaa zao. 41 Na mpaka wa urithi wao ulikuwa ni Sora, na Eshtaoli, na Irishemeshi; 42 na Shaalabini, na Aiyaloni, na Ithla; 43 na Eloni, na Timna, na Ekroni; 44 na Elteka, na Gibethoni, na Baalathi; 45 na Yehudi, na Bene-beraki, na Gathrimoni; 46 na Meyarkoni, na Rakoni, pamoja na huo mpaka uliokuwa mkabala wa Yafa. 47 Kisha mpaka wa wana wa Dani ulitokea kuwapita wao; kwa kuwa hao wana wa Dani wakakwea na kupigana na Leshemu, na kuutwaa, na kuupiga kwa makali ya upanga, na kuumiliki, nao wakakaa humo, wakauita Dani, kwa kuliandama jina la huyo Dani mzee wao. 48 Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Dani kwa kuandama jamaa zao; miji hii pamoja na vijiji vyake. 49 Basi wakamaliza hiyo kazi yao ya kuigawanya nchi iwe urithi kwa kuandama mipaka yake; kisha wana wa Israeli wakampa Yoshua, mwana wa Nuni, urithi katikati yao; 50 sawasawa na ile amri ya Bwana wakampa mji alioutaka, maana, ni Timnath-sera katika nchi ya vilima ya Efraimu; naye akaujenga huo mji na kukaa mumo. 51 Hizi ndizo nchi, ambazo Eleazari kuhani, na Yoshua huyo mwana wa Nuni, pamoja na hao vichwa vya nyumba za mababa ya kabila za wana wa Israeli, walizigawanya kwa njia ya kupiga kura, ziwe urithi, huko Shilo mbele ya Bwana, hapo mlangoni mwa hema ya kukutania. Basi hivyo wakamaliza kazi ya kuigawanya hiyo nchi.

Yoshua 20

1 Kisha Bwana akanena na Yoshua, na kumwambia, 2 Nena wewe na wana wa Israeli, uwaambie, Haya, toeni hiyo miji ya makimbilio, ambayo niliwaambia habari zake kwa mkono wa Musa; 3 ili kwamba mwenye kuua mtu, aliyemwua mtu awaye yote pasipo kukusudia, na pasipo kujua, apate kukimbilia kuko; nayo itakuwa ni mahali pa kukimbilia kwenu, kumkimbia huyo ajilipizaye kisasi cha damu. 4 Naye ataikimbilia miji hiyo mmojawapo, naye atasimama hapo penye maingilio ya lango la huo mji, kisha atanena neno lake masikioni mwa wazee wa mji; nao watamtia kwao ndani ya mji, na kumpa mahali, ili apate kukaa kati yao. 5 Na kama huyo mwenye kujilipiza kisasi cha damu akimwandamia, ndipo hawatamtoa huyo mwuaji kumtia mkononi mwake huyo; kwa sababu alimpiga mwenziwe naye hakujua, wala hakumchukia tangu hapo. 6 Naye atakaa katika mji huo, hata hapo atakaposimama mbele ya mkutano kuhukumiwa, hata kifo chake kuhani mkuu mwenye kuwapo siku hizo; ndipo yule mwuaji atarudi, na kuuendea mji wake mwenyewe, na nyumba yake mwenyewe, hata mji huo alioutoka hapo alipokimbia. 7 Nao wakaweka Kedeshi katika Galilaya katika nchi ya vilima ya Naftali, na Shekemu katika nchi ya vilima ya Efraimu, na Kiriath-arba (ndio Hebroni) katika nchi ya vilima ya Yuda. 8 Tena ng'ambo ya pili ya Yordani pande za Yeriko upande wa kuelekea mashariki wakaweka Bezeri ulioko nyikani, katika nchi tambarare ya kabila ya Reubeni, na Ramothi katika Gileadi katika kabila ya Gadi, na Golani katika Bashani katika kabila ya Manase. 9 Miji hiyo ndiyo miji iliyoamriwa kwa ajili ya wana wa Israeli wote, na kwa ajili ya mgeni akaaye kati yao ugenini, ili kwamba mtu awaye yote atakayemwua mtu pasipo kukusudia apate kimbilia huko, asife kwa mkono wa mwenye kujilipiza kisasi cha damu, hata hapo atakapokuwa amekwisha simama mbele ya mkutano.

Yoshua 21

1 Wakati huo hao vichwa vya nyumba za mababa ya Walawi wakamwendea Eleazari, kuhani, na Yoshua, mwana wa Nuni, na hao waliokuwa vichwa vya nyumba za mababa ya kabila za wana wa Israeli; 2 wakanena nao hapo Shilo katika nchi ya Kanaani, wakisema, Yeye Bwana aliamuru kwa mkono wa Musa kwamba sisi tupewe miji tupate kukaa humo, pamoja na malisho yake kwa ajili ya wanyama wetu wa mifugo. 3 Basi wana wa Israeli wakawapa Walawi miji hii, pamoja na malisho yake, katika urithi wao, sawasawa na hiyo amri ya Bwana. 4 Kura ikatokea kwa ajili ya jamaa za Wakohathi; na wana wa Haruni kuhani, waliokuwa katika Walawi, walipata miji kumi na mitatu kwa kura katika kabila ya Yuda, na katika kabila ya Simeoni, na katika kabila ya Benyamini. 5 Kisha Wakohathi wengine waliosalia walipata kwa kura katika jamaa za kabila ya Efraimu, na katika kabila ya Dani, na katika hiyo nusu ya kabila ya Manase, miji kumi. 6 Tena wana wa Gershoni walipata kwa kura katika jamaa za kabila ya Isakari, na katika kabila ya Asheri, na katika kabila ya Naftali, na katika hiyo nusu ya kabila ya Manase huko Bashani, miji kumi na mitatu. 7 Na wana wa Merari kwa kuandama jamaa zao walipata katika kabila ya Reubeni, na katika kabila ya Gadi, na katika kabila ya Zabuloni, miji kumi na miwili. 8 Kisha wana wa Israeli waliwapa Walawi kwa kura miji hiyo pamoja na malisho yake, kama Bwana alivyoamuru kwa mkono wa Musa. 9 Kisha wakawapa katika kabila ya wana wa Yuda, na katika kabila ya wana wa Simeoni, miji hii iliyotajwa hapa kwa majina; 10 nayo ilikuwa kwa ajili ya wana wa Haruni, wa jamaa ya Wakohathi, waliokuwa wa wana wa Lawi; kwa kuwa kura ya kwanza ilikuwa ni yao. 11 Nao wakawapa Kiriath-arba, huyo Arba alikuwa baba yake Anaki, (ndio Hebroni), katika nchi ya vilima ya Yuda, pamoja na malisho yake yaliyouzunguka pande zote. 12 Lakini mashamba ya mji, na vile vijiji vyake, wakampa Kalebu mwana wa Yefune kuwa milki yake. 13 Kisha wakawapa wana wa Haruni kuhani Hebroni pamoja na malisho yake, huo mji wa kukimbilia kwa ajili ya mwuaji, na Libna pamoja na malisho yake; 14 na Yatiri pamoja na malisho yake, na Eshtemoa pamoja na malisho yake; 15 na Holoni pamoja na malisho yake, na Debiri pamoja na malisho yake; 16 na Aini pamoja na malisho yake, na Yuta pamoja na malisho yake, na Bethshemeshi pamoja na malisho yake; miji kenda katika kabila hizo mbili. 17 Tena katika kabila ya Benyamini, Gibeoni pamoja na malisho yake, na Geba pamoja na malisho yake; 18 na Anathothi pamoja na malisho yake, na Almoni pamoja na malisho yake; miji minne. 19 Miji yote ya wana wa Haruni, makuhani, ilikuwa ni miji kumi na mitatu, pamoja na malisho yake. 20 Na jamaa za wana wa Kohathi, Walawi, hao wana wengine wa Kohathi waliosalia, wao walikuwa na miji ya kura yao katika kabila ya Efraimu. 21 Nao wakawapa Shekemu pamoja na malisho yake, katika nchi ya vilima ya Efraimu, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji; na Gezeri pamoja na malisho yake; 22 na Kibisaumu pamoja na malisho yake, na Beth-horoni pamoja na malisho yake, miji minne. 23 Tena katika kabila ya Dani Elteke pamoja na malisho yake, na Gibethoni pamoja na malisho yake; 24 na Aiyaloni pamoja na malisho yake, na Gath-rimoni pamoja na malisho yake; miji minne. 25 Tena katika hiyo nusu ya kabila ya Manase, Taanaki pamoja na malisho yake, na Gath-rimoni pamoja na malisho yake; miji miwili. 26 Miji yote ya jamaa za wana wa Kohathi waliosalia ilikuwa ni miji kumi, pamoja na malisho yake. 27 Tena wana wa Gershoni, katika jamaa za Walawi, waliwapa, katika hiyo nusu ya kabila ya Manase, Golani katika Bashani pamoja na malisho yake, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji; na Beeshtera pamoja na malisho yake; miji miwili. 28 Tena katika kabila ya Isakari, Kishioni pamoja na malisho yake, na Daberathi pamoja na malisho yake; 29 na Yarmuthi pamoja na malisho yake, na Enganimu pamoja na malisho yake; miji minne. 30 Tena katika kabila ya Asheri, Mishali pamoja na malisho yake, na Abdoni pamoja na malisho yake; 31 na Helkathi pamoja na malisho yake, na Rehobu pamoja na malisho yake; miji minne. 32 Tena katika kabila ya Naftali, Kedeshi katika Galilaya pamoja na malisho yake, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji, na Hamoth-dori pamoja na malisho yake, na Kartani pamoja na malisho yake; miji mitatu. 33 Miji yote ya Wagershoni kwa kuandama jamaa zao ilikuwa ni miji kumi na mitatu, pamoja na malisho yake. 34 Tena jamaa za wana wa Merari, hao Walawi waliosalia, katika kabila ya Zabuloni, Yokneamu pamoja na malisho yake, na Karta pamoja na malisho yake, 35 na Dimna pamoja na malisho yake, na Nahalali pamoja na malisho yake; miji minne. 36 Tena katika kabila ya Reubeni, Bezeri pamoja na malisho yake, na Yahasa pamoja na malisho yake, 37 na Kedemothi pamoja na malisho yake, na Mefaathi pamoja na malisho yake; miji minne. 38 Tena katika kabila ya Gadi Ramothi katika Gileadi pamoja na malisho yake, huo mji wa makimbilio kwa ajili ya mwuaji, na Mahanaimu pamoja na malisho yake; 39 na Heshboni pamoja na malisho yake, na Yazeri pamoja na malisho yake; jumla yake miji minne. 40 Miji hiyo yote ilikuwa ni miji ya wana wa Merari kwa kuandama jamaa zao, ni hizo jamaa za Walawi zilizosalia; na kura yao ilikuwa ni miji kumi na miwili. 41 Miji yote ya Walawi iliyokuwa kati ya milki ya wana wa Israeli ilikuwa ni miji arobaini na minane, pamoja na malisho yake. 42 Miji hiyo kila mmoja ulikuwa pamoja na malisho yake, yaliyouzunguka pande zote; ndivyo ilivyokuwa katika miji hiyo yote. 43 Basi Bwana aliwapa Israeli nchi hiyo yote, ambayo aliapa kwamba atawapa baba zao; nao wakaimiliki, na kukaa mumo. 44 Kisha Bwana akawapa raha pande zote, sawasawa na hayo yote aliyokuwa amewaapia baba zao; wala katika adui zao wote hakusimama hata mtu mmoja miongoni mwao mbele zao; yeye Bwana akawatia adui zao wote mikononi mwao. 45 Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo Bwana alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.

Yoshua 22

1 Wakati huo Yoshua akawaita Wareubeni, na Wagadi, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, 2 naye akawaambia, Ninyi mmeyaandama hayo yote mliyoamriwa na Musa, mtumishi wa Bwana, nanyi mmeisikia sauti yangu katika yote niliyowaamuru mimi; 3 hamkuwaacha hao ndugu zenu siku hizi nyingi hata hivi leo, lakini mmeyashika mausia ya amri ya Bwana, Mungu wenu. 4 Na sasa yeye Bwana, Mungu wenu, amewapa ndugu zenu kustarehe, kama alivyowaambia; basi sasa rudini ninyi mwende mahemani kwenu, hata nchi ya milki yenu, ambayo huyo Musa, mtumishi wa Bwana, aliwapa ng'ambo ya pili ya Yordani. 5 Lakini mjibidiishe sana kuzifanya amri na sheria, ambazo Musa, mtumishi wa Bwana, aliwaamuru, kumpenda Bwana, Mungu wenu, na kwenenda katika njia zake zote, na kuzishika amri zake, na kushikamana na yeye, na kumtumikia kwa moyo wenu wote na nafsi yenu yote. 6 Basi Yoshua akawabarikia, na kuwapa ruhusa waende zao; nao wakaenda mahemani kwao. 7 Basi Musa alikuwa amewapa hiyo nusu moja ya kabila ya Manase urithi katika Bashani; lakini hiyo nusu ya pili Yoshua aliwapa urithi kati ya ndugu zao, ng'ambo ya Yordani upande wa kuelekea magharibi. Zaidi ya hayo Yoshua, hapo alipowapeleka waende zao mahemani kwao, akawabarikia, 8 kisha akanena nao, na kuwaambia, Rudini na mali mengi mahemani kwenu, na ng'ombe wengi sana, na fedha, na dhahabu, na shaba, na chuma, na mavao mengi sana; mzigawanye na ndugu zenu hizo nyara za adui zenu. 9 Basi wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na hiyo nusu ya kabila ya Manase wakarudi, wakatoka kwa wana wa Israeli katika Shilo, ulioko nchi ya Kanaani, ili waende nchi ya Gileadi, hiyo nchi ya milki yao, waliyokuwa wanaimiliki, sawasawa na amri ya Bwana kwa mkono wa Musa. 10 Nao walipofika pande za Yordani, zilizo katika nchi ya Kanaani, hao wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na nusu ya kabila ya Manase, wakajenga madhabahu huko karibu na Yordani, iliyoonekana kuwa ni madhabahu kubwa. 11 Wana wa Israeli walisikia ikinenwa, Tazama, wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, wamejenga madhabahu huko upande wa mbele wa nchi ya Kanaani, katika nchi iliyo karibu na Yordani, kwa upande huo ulio milki ya wana wa Israeli. 12 Basi, wana wa Israeli waliposikia habari hiyo, mkutano wote wa wana wa Israeli wakakutanika pamoja huko Shilo, ili waende kupigana nao. 13 Kisha wana wa Israeli wakatuma wajumbe waende kwa wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, hata nchi ya Gileadi; nao ni hawa, Finehasi mwana wa Eleazari kuhani; 14 na pamoja naye wakuu kumi, mkuu mmoja wa nyumba ya mababa kwa ajili ya kila kabila ya Israeli; nao kila mmoja alikuwa ni kichwa cha nyumba ya mababa katika maelfu ya Israeli. 15 Nao wakawafikilia hao wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, katika nchi ya Gileadi, na wakasema nao, wakinena, 16 Mkutano wote wa Bwana wanena, Ni kosa gani hili mlilolikosa juu ya Mungu wa Israeli, hata mkakengeuka hivi leo na kuacha kumwandama Bwana, katika kujijengea madhabahu, na kuasi hivi leo juu ya Bwana? 17 Je! Ule uovu wa Peori haututoshi, ambao hamjajitakasa nafsi zenu katika huo hata hivi leo, ijapokuwa ilikuja tauni juu ya mkutano wa Bwana, 18 hata ikawa hamna budi hivi leo kugeuka na kuacha kumwandama Bwana? Kisha itakuwa, kwa kuwa ninyi mwamwasi Bwana hivi leo, kwamba kesho yeye atakasirika na mkutano wote wa Israeli. 19 Basi kwamba hiyo nchi ya milki yenu si tohara, ndipo ninyi vukeni na kuingia nchi ya milki yake Bwana, ambayo maskani ya Bwana inakaa ndani yake, nanyi twaeni milki kati yetu; lakini msimwasi Bwana, wala msituasi sisi, kwa kujijengea madhabahu zaidi ya hiyo madhabahu ya Bwana, Mungu wetu. 20 Je! Huyo Akani mwana wa Zera hakukosa katika vile vitu vilivyowekwa wakfu, na hasira ikauangukia mkutano wote wa Israeli? Kisha mtu huyo hakuangamia peke yake katika uovu wake? 21 Ndipo hapo wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na hiyo nusu ya kabila ya Manase, wakajibu, na kuwaambia hao waliokuwa ni vichwa vya maelfu ya Israeli, wakasema, 22 Mungu, Mungu Bwana, naam, Mungu, Mungu Bwana, yeye yuajua, na Israeli naye atajua; kama ni katika uasi, au kama ni katika kosa juu ya Bwana, (usituokoe hivi leo); 23 sisi kujijengea madhabahu ili kukengeuka na kuacha kumwandama Bwana; au kama ni kusongeza juu yake sadaka ya kuteketezwa, au sadaka ya unga, au kama ni kusongeza sadaka za amani juu yake, yeye Bwana mwenyewe na alitake jambo hili; 24 au kama sisi tumefanya jambo hili kwa hadhari sana, tena makusudi, huku tukisema, Katika siku zijazo wana wenu yamkini wakanena na wana wetu, na kusema, Ninyi mna nini na Bwana, yeye Mungu wa Israeli? 25 Kwa kuwa yeye Bwana ameufanya huu mto wa Yordani uwe mpaka katikati ya sisi na ninyi, enyi wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, hamna fungu katika Bwana; basi hivyo wana wenu wangewakomesha wana wetu wasimche Bwana. 26 Kwa ajili ya hayo tulisema, Na tufanye tayari ili kujijengea madhabahu, si kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa, wala kwa sadaka yo yote; 27 bali itakuwa ni ushahidi kati ya sisi na ninyi, tena kati ya vizazi vyetu baada yetu, ili kwamba tufanye huo utumishi wa Bwana mbele yake kwa njia ya sadaka zetu za kuteketezwa, na kwa dhabihu zetu, na kwa sadaka zetu za amani; ili kwamba wana wenu wasiwaambie wana wetu katika zamani zijazo, Ninyi hamna fungu katika Bwana. 28 Kwa hiyo tulisema, Itakuwa, hapo watakapotuambia neno kama hilo, au kuwaambia watu wa vizazi vyetu katika zamani zijazo neno kama hilo, ndipo sisi tutawaambia, Angalieni huu mfano wa madhabahu ya Bwana, walioufanya baba zetu, si kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa, wala kwa ajili ya dhabihu; lakini ni ushahidi kati ya sisi na ninyi. 29 Mungu na atuzuie msimwasi Bwana, na kukengeuka hivi leo na kuacha kumwandama Bwana, hata mkajenga madhabahu kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa, au sadaka za unga, au dhabihu, mbali na ile madhabahu ya Bwana, Mungu wetu, iliyo huko mbele ya maskani yake. 30 Basi Finehasi kuhani, na wakuu wa mkutano, maana, ni hao waliokuwa vichwa vya maelfu ya Israeli waliokuwa pamoja naye, hapo walipoyasikia hayo maneno waliyoyasema hao wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na wana wa Manase, maneno hayo yaliwaridhia sana. 31 Naye Finehasi, mwana wa Eleazari, kuhani, akawaambia wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, na wana wa Manase, akasema, Siku hii ya leo twajua ya kwamba Bwana yu kati yetu, kwa sababu hamkukosa katika jambo hili mbele ya Bwana; sasa ninyi mmewaokoa wana wa Israeli na mkono wa Bwana. 32 Kisha Finehasi, mwana wa Eleazari, kuhani, na hao wakuu, wakarudi na kuwaacha wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, wakatoka katika nchi ya Gileadi, na kuingia nchi ya Kanaani; wakawarudia wana wa Israeli, wakawapa habari. 33 Wana wa Israeli nao wakaliridhia jambo hilo; nao wana wa Israeli wakamhimidi Mungu, wala hawakusema tena habari ya kuwaendea juu yao kupigana nao, wala kuiharibu nchi waliyoikaa wana wa Reubeni, na wana wa Gadi. 34 Basi hao wana wa Reubeni, na wana wa Gadi, wakaiita madhabahu hiyo Edi; wakasema, Kwa kuwa ni ushahidi kati yetu ya kwamba yeye Bwana ndiye Mungu.

Yoshua 23

1 Hata ikawa baada ya siku nyingi, Bwana alipokuwa amekwisha kuwapa Israeli raha mbele ya adui zao pande zote, naye Yoshua alipokuwa mzee, mwenye miaka mingi sana, 2 Yoshua akawaita Israeli wote, wazee wao, na wakuu wao, na makadhi yao, na maakida yao, akawaambia, Mimi ni mzee, nami nimekwendelea sana katika miaka yangu; 3 nanyi mmeona mambo yote ambayo Bwana, Mungu wenu, amewatenda mataifa haya yote kwa ajili yenu; kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye aliyewapigania ninyi. 4 Tazama, nimewagawieni kwa kura mataifa haya yaliyobaki, yawe urithi kwa kabila zenu, toka mto wa Yordani, pamoja na mataifa yote niliyowakatilia mbali, mpaka bahari kubwa upande wa machweo ya jua. 5 Yeye Bwana, Mungu wenu, atawatoa kwa nguvu mbele yenu, atawafukuza wasiwe mbele ya macho yenu tena; nanyi mtaimiliki nchi yao, kama Bwana Mungu wenu, alivyowaambia. 6 Basi, iweni mashujaa sana kuyashika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati ya Musa, na kuyatenda, msiyaache kwa kugeukia upande wa kuume wala upande wa kushoto. 7 Msiingie kati ya mataifa haya, yaani, haya yaliyobaki kati yenu; wala msitaje majina ya miungu yao, wala kuwaapisha watu kwa majina hayo, wala kuitumikia, wala kujiinamisha mbele yao; 8 bali shikamaneni na Bwana, Mungu wenu, kama mlivyotenda hata hivi leo. 9 Maana Bwana amefukuza mbele yenu mataifa walio hodari, kisha wenye nguvu, lakini kwenu ninyi hapana mtu aliyesimama mbele yenu hata leo. 10 Mtu mmoja miongoni mwenu atafukuza watu elfu; maana Bwana, Mungu wenu, ndiye anayewapigania, kama alivyowaambia. 11 Jihadharini nafsi zenu, basi, ili mmpende Bwana, Mungu wenu. 12 Lakini mkirudi nyuma kwa njia yo yote na kushikamana na mabaki ya mataifa, yaani, mataifa haya yaliyobaki kati yenu, na kuoana nao, na kuingia kwao, nao kuingia kwenu; 13 jueni hakika ya kuwa Bwana, Mungu wenu, hatawafukuza tena mataifa haya mbele ya macho yenu, bali watakuwa mtego kwenu na tanzi, na mjeledi mbavuni mwenu, na miiba machoni mwenu, hata mtakapoangamia na kutoka katika nchi hii njema, ambayo Bwana, Mungu wenu, amewapa ninyi. 14 Angalieni, mimi leo ninakwenda njia ile waendayo watu wote wa ulimwengu; nanyi nyote mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena Bwana, Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu hapana neno lo lote mlilopungukiwa. 15 Kisha itakuwa, kama yalivyowafikilia yale mambo mema yote, Bwana, Mungu wenu, aliyowaahidia ninyi, kadhalika Bwana atawafikilizia mabaya yote, hata atakapokuwa amewaangamiza katika nchi hii njema, Bwana Mungu wenu, aliyowapa. 16 Hapo mtakapolivunja agano la Bwana, Mungu wenu, alilowaamuru, na kwenda kuitumikia miungu mingine, na kujiinamisha mbele yao, ndipo hasira ya Bwana itakapowaka juu yenu, nanyi mtaangamia upesi katika nchi hii njema aliyowapa.

Yoshua 24

1 Yoshua akawakusanya kabila zote za Israeli huko Shekemu, akawaita wazee wa Israeli, na wakuu wao, na waamuzi wao, na maakida wao nao wakahudhuria mbele za Mungu. 2 Yoshua akawaambia watu wote, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Baba zenu hapo zamani walikaa ng'ambo ya Mto, maana Tera, baba yake Ibrahimu, naye ni baba yake Nahori; wakaitumikia miungu mingine. 3 Nami nikamtwaa Ibrahimu baba yenu toka ng'ambo ya Mto, nikamwongoza katika nchi yote ya Kanaani; nikaongeza uzao wake, nikampa Isaka. 4 Kisha nikampa huyo Isaka, Yakobo na Esau; nami nikampa Esau mlima Seiri aumiliki; Yakobo na watoto wake wakashuka Misri. 5 Kisha nikawatuma Musa na Haruni nikaipiga nchi ya Misri, kwa hayo yote niliyoyatenda kati yake; hatimaye nikawatoa ninyi. 6 Nikawatoa baba zenu watoke Misri; nanyi mkaifikilia bahari; Wamisri wakawafuatia baba zenu kwa magari na wapanda farasi mpaka bahari ya Shamu. 7 Nao walipomlilia Bwana, akaweka giza kati ya ninyi na Wamisri, akaileta bahari juu yao, akawafunikiza; nayo macho yenu yaliyaona mambo niliyoyatenda huko Misri; kisha mkakaa jangwani siku nyingi. 8 Kisha nikawaleta na kuwaingiza katika nchi ya Waamori waliokaa ng'ambo ya pili ya Yordani; nao wakapigana nanyi; nikawatia mikononi mwenu, mkaimiliki nchi yao; nami nikawaangamiza mbele yenu. 9 Ndipo Balaki, mwana wa Sipori, mfalme wa Moabu, akainuka, akapigana na Israeli; tena akatuma watu akamwita Balaamu, mwana wa Beori, aje awalaani; 10 lakini sikukubali kumsikiliza Balaamu; kwa hiyo akafuliza kuwabarikia ninyi; basi nikawatoa katika mkono wake. 11 Nanyi mliuvuka Yordani, mkafika Yeriko; nao watu wa Yeriko wakapigana nanyi, Mwamori, na Mperizi, na Mkanaani, na Mhiti, na Mgirgashi, na Mhivi, na Myebusi; nami nikawatia mikononi mwenu. 12 Nikatuma mavu mbele yenu, waliowafukuza mbele yenu hao wafalme wawili wa Waamori, si kwa upanga wako, wala kwa upinde wako. 13 Nami nimewapa ninyi nchi msiyoitendea kazi, na miji msiyoijenga, nanyi mmekaa humo; mnakula matunda ya mashamba ya mizabibu na mizeituni msiyoipanda. 14 Basi sasa mcheni Bwana, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye Bwana. 15 Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia Bwana, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana. 16 Hao watu wakajibu wakasema, Hasha! Tusimwache Bwana, ili kuitumikia miungu mingine; 17 kwa maana Bwana, Mungu wetu, yeye ndiye aliyetupandisha sisi na baba zetu kutoka nchi ya Misri; kutoka nyumba ya utumwa; naye ndiye aliyezifanya ishara zile kubwa mbele ya macho yetu, na kutulinda katika njia ile yote tuliyoiendea, na kati ya watu wa mataifa yote tuliopita katikati yao. 18 Bwana ndiye aliyewafukuza watu wa mataifa yote watoke mbele yetu, naam, Waamori waliokaa katika nchi hii; basi, kwa sababu hiyo sisi nasi tutamtumikia Bwana, maana yeye ndiye Mungu wetu. 19 Yoshua akawaambia watu, Hamwezi kumtumikia Bwana; kwa kuwa yeye ni Mungu mtakatifu; yeye ni Mungu mwenye wivu; hatawasamehe makosa yenu, wala dhambi zenu. 20 Kama mkimwacha Bwana na kuitumikia miungu migeni, ndipo atageuka na kuwatenda mabaya na kuwaangamiza, baada ya kuwatendea mema. 21 Lakini hao watu wakamwambia Yoshua, La! Lakini tutamtumikia Bwana. 22 Yoshua akawaambia watu, Ninyi mmekuwa mashahidi juu ya nafsi zenu, ya kuwa mmemchagua Bwana, ili kumtumikia yeye. Wakasema, Sisi tu mashahidi. 23 Akasema, Basi sasa, iondoeni miungu migeni iliyo kati yenu, mkaielekeze mioyo yenu kwa Bwana, Mungu wa Israeli. 24 Ndipo hao watu wakamwambia Yoshua, Bwana, Mungu wetu, ndiye tutakayemtumikia; na sauti yake ndiyo tutakayoitii. 25 Basi Yoshua akafanya agano na wale watu siku ile, akawapa amri na agizo huko Shekemu. 26 Yoshua akayaandika maneno haya katika kitabu cha torati ya Mungu; kisha akatwaa jiwe kubwa, akalisimamisha huko, chini ya ule mwaloni uliokuwa karibu na patakatifu pa Bwana. 27 Yoshua akawaambia watu wote, Tazama, jiwe hili litakuwa shahidi juu yetu; kwa maana limesikia maneno yote ya Bwana aliyotuambia, basi litakuwa shahidi juu yenu, msije mkamkana Mungu wenu. 28 Basi Yoshua akawaruhusu watu, wakaenda zao, kila mtu kwenye urithi wake. 29 Ikawa, baada ya hayo, Yoshua, mwana wa Nuni, mtumishi wa Bwana, akafa, mwenye umri wa miaka mia na kumi. 30 Wakamzika katika mpaka wa urithi wake, huko Timnath-sera; ulio katika nchi ya vilima ya Efraimu, upande wa kaskazini wa mlima wa Gaashi. 31 Nao Israeli wakamtumikia Bwana siku zote za Yoshua, na siku zote za hao wazee walioishi baada ya kufa kwake Yoshua, hao walioijua kazi yote ya Bwana, aliyowatendea Israeli. 32 Na hiyo mifupa ya Yusufu, ambayo wana wa Israeli walikuwa wameileta kutoka Misri, wakaizika huko Shekemu katika ile sehemu ya nchi, Yakobo aliyoinunua kwa wana wa Hamori, babaye Shekemu, kwa vipande mia vya fedha; nayo ikawa ni urithi wa wana wa Yusufu. 33 Huyo Eleazari mwana wa Haruni naye akafa; wakamzika katika kilima cha Finehasi mwanawe, ambacho alipewa yeye katika nchi ya vilima ya Efraimu.

Waamuzi 1

1 Ikawa baada ya kufa kwake Yoshua, wana wa Israeli wakamwuliza Bwana, wakisema, Ni nani atakayekwea kwanza kwa ajili yetu juu ya Wakanaani, ili kupigana nao? 2 Bwana akasema, Yuda atakwea; tazama, nimeitia hiyo nchi mkononi mwake. 3 Ndipo Yuda akamwambia Simeoni ndugu yake, Kwea wewe pamoja nami katika kura yangu, ili tupate kupigana na Wakanaani; kisha mimi nami nitakwenda pamoja nawe katika kura yako. Basi Simeoni akaenda pamoja naye. 4 Yuda akakwea; naye Bwana akawatia Wakanaani na Waperizi mkononi mwao; nao wakawapiga huko Bezeki watu elfu kumi. 5 Wakampata huyo Adoni-bezeki huko Bezeki; wakapigana naye, nao wakawapiga Wakanaani na Waperizi. 6 Lakini Adoni-bezeki akakimbia; nao wakamwandamia na kumshika, wakamkata vyanda vyake vya gumba vya mikono na vya miguu. 7 Adoni-bezeki akasema, Wafalme sabini, waliokuwa wamekatwa vyanda vyao vya gumba vya mikono na vya miguu, waliokota chakula chao chini ya meza yangu; kama nilivyofanya mimi, Mungu amenilipa vivyo. Wakamleta Yerusalemu naye akafa kuko. 8 Kisha wana wa Yuda wakapigana na Yerusalemu, wakautwaa, wakaupiga kwa makali ya upanga, na kuupiga moto huo mji. 9 Baadaye wana wa Yuda wakatelemka ili wapigane na hao Wakanaani waliokaa katika nchi ya milimani, na nchi ya Negebu, na nchi ya Shefela. 10 Kisha Yuda akawafuatia hao Wakanaani waliokaa katika Hebroni; (jina la Hebroni hapo kwanza ulikuwa ukiitwa Kiriath-arba;) nao wakamwua Sheshai, na Ahimani, na Talmai. 11 Kisha kutoka hapo akawafuatia wale wenye kukaa Debiri. (Jina la Debiri hapo kwanza ulikuwa ukiitwa Kiriath-seferi.) 12 Huyo Kalebu alisema, Yeye atakayeupiga Kiriath-seferi na kuutwaa, nitamwoza mwanangu Aksa awe mkewe. 13 Naye Othnieli, mwana wa Kenazi, ndugu mdogo wa huyo Kalebu, aliutwaa; basi akamwoza mwanawe Aksa. 14 Ikawa hapo alipokwenda kukaa naye, huyo mwanamke akamtaka ili aombe shamba kwa baba yake; na huyo mwanamke akashuka katika punda wake; Kalebu akamwuliza, Una haja gani utakayo? 15 Mwanamke akasema, Nipe baraka; kwa kuwa wewe umeniweka katika nchi ya Negebu, basi unipe na vijito vya maji pia. Kalebu akampa vile vijito vya maji vya juu na vijito vya chini. 16 Hao wana wa Mkeni, huyo shemeji yake Musa, wakakwea juu kutoka katika huo mji wa mitende, pamoja na wana wa Yuda, na kuingia hiyo nyika ya Yuda, iliyo upande wa kusini wa Aradi; nao wakaenda na kukaa pamoja na watu hao. 17 Kisha Yuda akaenda pamoja na nduguye Simeoni, na wakawapiga Wakanaani waliokaa katika Sefathi, na kuuharibu mji kabisa. Na jina la mji huo ulikuwa ukiitwa Horma. 18 Pamoja na haya Yuda aliutwaa Gaza pamoja na mipaka yake, na Ashkeloni na mipaka yake, na Ekroni na mipaka yake. 19 Bwana alikuwa pamoja na Yuda; naye akawafukuza watu waliokaa katika nchi ya milimani; asiweze kuwafukuza hao waliokaa katika hilo bonde, kwa kuwa wao walikuwa na magari ya chuma. 20 Kisha wakampa huyo Kalebu Hebroni, kama alivyonena Musa naye akawafukuza wale wana watatu wa Anaki. 21 Lakini wana wa Benyamini hawakuwafukuza Wayebusi waliokaa mji wa Yerusalemu; bali Wayebusi walikaa pamoja na wana wa Benyamini ndani ya Yerusalemu hata hivi leo. 22 Nyumba ya Yusufu nayo, wao nao walikwea kwenda juu ya Betheli; naye Bwana alikuwa pamoja nao. 23 Kisha mbari ya Yusufu wakatuma watu waende kuupeleleza Betheli. (Jina la mji huo hapo kwanza ulikuwa ukiitwa Luzu.) 24 Hao wapelelezi walimwona mtu atoka katika huo mji, wakamwambia, Tafadhali, utuonyeshe maingilio ya mji huu, nasi tutakutendea mema. 25 Basi akawaonyesha maingilio ya mji, nao wakaupiga huo mji kwa makali ya upanga; lakini huyo mtu walimwacha aende zake, na watu wote wa jamaa yake. 26 Huyo mtu akaenda katika nchi ya Wahiti, akajenga mji, akaliita jina la huo mji Luzu; nalo ndilo jina lake hata hivi leo. 27 Tena Manase hakuwatoa wenyeji wa Bethsheani na miji yake, wala hao waliokaa Taanaki na miji yake, wala hao waliokaa Dori na miji yake, wala hao waliokaa Ibleamu na miji yake, wala hao waliokaa Megido na miji yake; lakini hao Wakanaani walikuwa hawakukubali kuiacha nchi hiyo. 28 Kisha ikawa, hapo Israeli walipokuwa wamepata nguvu, ndipo walipowatia hao Wakanaani katika kazi ya shokoa, wala hawakuwafukuza kabisa. 29 Efraimu naye hakuwatoa Wakanaani waliokuwa wakikaa katika Gezeri; lakini Wakanaani walikaa ndani ya Gezeri kati yao. 30 Zabuloni naye hakuwatoa wenyeji wa Kitroni, wala hao waliokaa katika Nahalali; lakini Wakanaani walikaa kati yao, wakalazimishwa shokoa. 31 Asheri naye hakuwatoa wenyeji wa Aka, wala hao waliokaa Sidoni, wala hao wa Alabu, wala hao wa Akzibu, wala hao wa Helba, wala hao wa Afeka, wala hao wa Rehobu; 32 lakini Waasheri wakakaa kati ya Wakanaani, hao wenyeji wa nchi; kwa kuwa hawakuwafukuza. 33 Naftali naye hakuwatoa wenyeji wa Bethshemeshi, wala hao waliokaa Bethanathi; lakini alikaa kati ya Wakanaani, hao wenyeji wa nchi; pamoja na haya hao wenyeji wa Bethshemeshi, na wenyeji wa Bethanathi, wakawatumikia kazi ya shokoa. 34 Kisha Waamori waliwasukumiza wana wa Dani waende milimani; kwani hawakuwakubali kutelemkia bondeni; 35 lakini hao Waamori waliendelea kukaa katika kilima cha Heresi, na katika Aiyaloni, na katika Shaalbimu; pamoja na haya mkono wa hiyo nyumba ya Yusufu ulishinda, hata wakawalazimisha shokoa. 36 Mpaka wa Waamori ulikuwa tangu huko kupandia Akrabimu, tangu hilo jabali, na juu yake.

Waamuzi 2

1 Kisha malaika wa Bwana alikwea juu kutoka Gilgali kwenda Bokimu. Akasema, Mimi nimewaleta ninyi mkwee juu kutoka nchi ya Misri, nami nimewaleta hata nchi niliyowaapia baba zenu; nami nilisema, Mimi milele sitalivunja hilo agano langu nililoagana nanyi; 2 nanyi msifanye agano lo lote na hawa wenyeji wa nchi hii; zipomosheni nchi madhabahu zao; lakini hamkuisikia sauti yangu; je! Mmefanya haya kwa sababu gani? 3 Basi kwa ajili ya hayo mimi nilisema zaidi, Mimi sitawafukuza watoke mbele zenu; lakini watakuwa kama miiba mbavuni mwenu, na miungu yao itakuwa ni tanzi kwenu. 4 Ikawa, hapo huyo malaika wa Bwana alipoyanena maneno haya, kuwaambia wana wa Israeli wote, ndipo hao watu wakainua sauti zao na kulia. 5 Nao wakaliita jina la mahali pale Bokimu; nao wakamchinjia Bwana sadaka huko. 6 Basi hapo Yoshua alipowapa watu ruhusa waende zao, wana wa Israeli wakaenda kila mtu kuuendea urithi wake, ili kuimiliki hiyo nchi. 7 Watu hao wakamtumikia Bwana siku zote za Yoshua, na siku zote za hao wazee walioendelea siku zao baada ya Yoshua, hao waliokuwa wameiona hiyo kazi kubwa ya Bwana yote, aliyokuwa ameitenda kwa ajili ya Israeli. 8 Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Bwana, akafa, naye alipata umri wa miaka mia na kumi. 9 Nao wakamzika katika mpaka wa urithi wake katika Timnath-heresi, katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu, upande wa kaskazini wa mlima wa Gaashi. 10 Tena watu wote wa kizazi hicho nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao, ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda kwa ajili ya Israeli. 11 Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za macho ya Bwana, nao wakawatumikia Mabaali. 12 Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao; wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika. 13 Wakamwacha Bwana, wakamtumikia Baali na Maashtorethi. 14 Hasira ya Bwana ikawaka juu ya Israeli, naye akawatia katika mikono ya watu waliowateka nyara, akawauza na kuwatia katika mikono ya adui zao pande zote; hata wasiweze tena kusimama mbele ya adui zao. 15 Kila walikokwenda mkono wa Bwana ulikuwa juu yao kuwatenda mabaya, kama Bwana alivyosema, na kama Bwana alivyowaapia; nao wakafadhaika sana. 16 Kisha Bwana akawainua waamuzi, waliowaokoa na mikono ya watu hao waliowateka nyara. 17 Lakini hawakuwasikiliza hao waamuzi wao, maana walifanya uasherati kwa kuifuata miungu mingine, wakajiinamisha mbele yao; wakageuka upesi, na kuiacha njia ile waliyoiendea baba zao, waliozitii amri za Bwana bali wao hawakufanya hivyo. 18 Na wakati Bwana alipowainulia waamuzi, ndipo Bwana alikuwa pamoja na mwamuzi huyo, akawaokoa na mikono ya adui zao siku zote za mwamuzi huyo; maana Bwana alighairi kwa ajili ya kuugua kwao kwa sababu ya watu wale waliowaonea na kuwasumbua. 19 Lakini ikawa, wakati alipokufa mwamuzi huyo, wakarudi nyuma wakafanya maovu kuliko baba zao, kwa kuifuata miungu mingine ili kuitumikia, na kuinama mbele yao; hawakuacha matendo yao, wala njia zao za ukaidi. 20 Basi hasira ya Bwana ikawaka juu ya Israeli, naye akasema, Kwa kuwa taifa hili wamelihalifu agano langu nililowaamuru baba zao, wala hawakuisikiliza sauti yangu; 21 mimi nami tokea sasa sitalifukuza taifa mojawapo la hayo aliyoyaacha Yoshua alipokufa; 22 ili kwa njia ya hayo nipate kuwajaribu Israeli, kwamba wataishika njia ya Bwana kwenda katika njia hiyo, au sivyo. 23 Basi Bwana akawaacha mataifa yale, wala hakuwafukuza kwa upesi, wala hakuwatia katika mikono ya Yoshua.

Waamuzi 3

1 Basi haya ndiyo mataifa ambao Bwana aliwaacha, ili awajaribu Israeli kwa hao, yaani, awajaribu hao wote ambao hawakuvijua vita vyote vya Kanaani; 2 ili kwamba vizazi vya wana wa Israeli wapate kujua ili kuwafundisha vita, hasa wao ambao hawakujua vita kabla ya wakati ule; 3 aliwaacha wakuu watano wa Wafilisti, na Wakanaani wote, na Wasidoni, na Wahivi waliokaa katika kilima cha Lebanoni, toka mlima wa Baal-hermoni mpaka kuingia Hamathi. 4 Naye aliwaacha ili awajaribu Israeli kwa hao, apate kujua kwamba watasikiliza amri za Bwana, alizowaamuru baba zao, kwa mkono wa Musa. 5 Basi wana wa Israeli wakaketi kati ya Wakanaani; hao Wahiti, na hao Waamori, na hao Waperizi, na hao Wahivi na hao Wayebusi; 6 wakawaoa binti zao, na binti zao wenyewe wakawaoza wana wao waume, na kuitumikia miungu yao. 7 Wana wa Israeli walifanya yaliyo maovu mbele za macho ya Bwana, nao wakamsahau Bwana, Mungu wao, nao wakawatumikia Mabaali na Maashtorethi. 8 Kwa hiyo hasira za Bwana ziliwaka juu ya Israeli, naye akawauza na kuwatia mikononi mwa Kushan-rishathaimu mfalme wa Mesopotamia; na wana wa Israeli wakamtumikia huyo Kushan-rishathaimu muda wa miaka minane. 9 Kisha wana wa Israeli walipomlingana Bwana, Bwana akawainulia wana wa Israeli mwokozi, aliyewaokoa, yaani, Othnieli mwana wa Kenazi, ndugu mdogo wa Kalebu. 10 Roho ya Bwana ikamjilia juu yake, naye akawa mwamuzi wa Israeli; akatoka kwenenda vitani, naye Bwana akamtia huyo Kushan-rishathaimu, mfalme wa Mesopotamia, mkononi mwake; na mkono wake ukamshinda Kushan-rishathaimu. 11 Nayo nchi ikawa na amani muda wa miaka arobaini. Kisha Othnieli, mwana wa Kenazi, akafa. 12 Basi wana wa Israeli walifanya yaliyo maovu tena mbele za Bwana; naye Bwana akamtia nguvu Egloni mfalme wa Moabu juu ya Israeli, kwa sababu walikuwa wameyafanya yaliyo maovu mbele za macho ya Bwana. 13 Huyo Egloni akakutanisha kwake wana wa Amoni na Amaleki; akaenda na kuwapiga Israeli, nao wakauchukua huo mji wa mitende. 14 Wana wa Israeli walimtumikia Egloni mfalme wa Moabu muda wa miaka kumi na minane. 15 Lakini wana wa Israeli walipomlilia Bwana, Bwana akawainulia mwokozi, Ehudi, mwana wa Gera, Mbenyamini, mtu aliyekuwa mwenye shoto; nao wana wa Israeli walimpelekea Egloni mfalme wa Moabu tunu mkononi mwa huyo Ehudi. 16 Ehudi alijifanyia upanga uliokuwa na makali kuwili, urefu wake ulipata dhiraa moja; akaufunga huo upanga ndani ya nguo yake katika paja lake la mkono wa kuume. 17 Kisha akamsongezea Egloni, mfalme wa Moabu, hiyo tunu; basi Egloni alikuwa ni mtu aliyewanda sana. 18 Naye hapo alipokuwa amekwisha kuisongeza hiyo tunu, akawapa ruhusa watu hao walioichukua tunu, wakaenda zao. 19 Lakini yeye mwenyewe akageuka kutoka huko kwenye sanamu zilizokuwa karibu na Gilgali, akasema, Mimi nina ujumbe wa siri kwako wewe, Ee mfalme. Naye akasema, Nyamazeni kimya. Watu wote waliokuwa wanasimama karibu naye wakatoka na kumwacha. 20 Basi Ehudi akamwendea; naye alikuwa anaketi peke yake katika chumba chake cha baridi. Ehudi akasema, Mimi nina ujumbe utokao kwa Mungu kwako wewe. Basi akainuka katika kiti chake. 21 Ehudi akaunyosha mkono wake wa kushoto, akaushika huo upanga kuutoa hapo katika paja lake la kuume, akamtia tumboni mwake; 22 hicho kipini nacho kikaingia ndani pamoja na huo upanga wenyewe; nayo mafuta yakashikamana tena juu ya upanga, kwani hakuutoa tena upanga tumboni; nao ukatokea kwa nyuma. 23 Ndipo Ehudi akatoka nje barazani, akamfungia milango ya hicho chumba na kuifunga kwa ufunguo. 24 Basi alipokuwa amekwisha toka nje, hao watumishi wake wakaenda; wakaona, na tazama, hiyo milango ya chumba ilikuwa imefungwa kwa ufunguo; nao wakasema, Hapana budi amejifunika miguu yake ndani ya chumba cha baridi. 25 Wakangoja hata wakatahayari; na tazama, hakuifungua milango ya chumba; basi wakatwaa ufunguo, na kuifungua; na tazama, bwana wao alikuwa ameanguka nchi, naye amekufa. 26 Naye Ehudi alikimbia hapo walipokuwa wakingoja, akapita huko kwenye sanamu, na kukimbilia Seira. 27 Ikawa, hapo alipofika akapiga tarumbeta katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu, ndipo wana wa Israeli wakatelemka pamoja naye kutoka huko milimani, naye akawatangulia. 28 Akawaambia, Niandameni mimi; kwa kuwa Bwana amewatia adui zenu, Wamoabi, mikononi mwenu. Basi wakatelemka na kumfuata, wakavishika vivuko vya Yordani kinyume cha Wamoabi, wala hawakumwacha mtu kuvuka. 29 Wakati huo wakapiga katika Wamoabi watu waume wapata kama elfu kumi, ambao wote walikuwa wanene, na wote mashujaa; hakupona hata mtu mmoja. 30 Basi Moabu alishindwa siku hiyo chini ya mikono ya Israeli. Nayo nchi ikawa na amani muda wa miaka themanini 31 Tena baada yake huyo alikuwapo Shamgari mwana wa Anathi, aliyepiga katika Wafilisti watu mia sita kwa konzo la ng'ombe; yeye naye aliwaokoa Israeli.

Waamuzi 4

1 Hata alipokufa Ehudi, wana wa Israeli wakafanya yaliyo maovu tena mbele za macho ya Bwana. 2 Bwana akawauza na kuwatia katika mkono wa Yabini, mfalme wa Kanaani, aliyetawala huko Hazori; na Sisera, aliyekaa katika Haroshethi wa Mataifa, alikuwa amiri wa jeshi lake. 3 Wana wa Israeli wakamlilia Bwana; kwa kuwa Sisera alikuwa na magari ya chuma mia kenda; naye akawaonea wana wa Israeli kwa nguvu muda wa miaka ishirini. 4 Basi Debora, nabii mke, mkewe Lapidothi, ndiye aliyekuwa mwamuzi wa Israeli wakati ule. 5 Naye alikaa chini ya mtende wa Debora, kati ya Rama na Betheli, katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu; wana wa Israeli wakakwea kwake, awaamue. 6 Huyo akatuma mtu akamwita Baraka wa Abinoamu toka Kedesh-Naftali, akamwambia, Je! Bwana, Mungu wa Israeli, hakutoa amri, akisema, Enenda, ukawavute kwako, huko katika mlima wa Tabori, watu elfu kumi wa wana wa Naftali, na wa wana wa Zabuloni? 7 Nami nitakuvutia Sisera, amiri wa jeshi lake Yabini, hata mto wa Kishoni, pamoja na magari yake, na wingi wa watu wake; nami nitamtia mkononi mwako. 8 Baraka akamwambia, Kama utakwenda pamoja nami ndipo nitakwenda; bali kama huendi pamoja nami, mimi siendi. 9 Basi akasema, Hakika nitakwenda pamoja nawe, lakini safari utakayoiendea haitakupatia heshima wewe; maana Bwana atamwuza Sisera katika mkono wa mwanamke. Debora akainuka, akaenda pamoja na Baraka mpaka Kedeshi. 10 Baraka akawakutanisha Naftali na Zabuloni waende Kedeshi wakakwea watu elfu kumi wakimfuata; Debora naye akaenda pamoja naye. 11 Basi Heberi, Mkeni, alikuwa amejitenga na Wakeni, yaani na wana wa Hobabu, shemeji yake Musa, akaipiga hema yake mbali penye mwaloni ulioko Saanaimu, karibu na Kedeshi. 12 Watu wakamwambia Sisera ya kwamba Baraka, mwana wa Abinoamu amekwea kwenda mlima wa Tabori. 13 Sisera akayakusanya magari yake yote, naam, magari ya chuma mia kenda, na watu wote waliokuwa pamoja naye, toka Haroshethi wa Mataifa mpaka mto wa Kishoni. 14 Debora akamwambia Baraka, Haya! Inuka; maana siku hii ndiyo siku ambayo Bwana amemtia Sisera katika mkono wako. Je! Bwana hakutoka atangulie mbele yako? Basi Baraka akashuka katika mlima wa Tabori, na watu elfu kumi wakamfuata. 15 Bwana akamfadhaisha Sisera na magari yake yote, na jeshi lake lote, kwa makali ya upanga, mbele ya Baraka; basi Sisera akashuka katika gari lake, akakimbia kwa miguu. 16 Lakini Baraka akayafuatia magari, na jeshi, hata Haroshethi wa Mataifa; na hilo jeshi lote la Sisera likaanguka kwa makali ya upanga; hakusalia hata mtu mmoja. 17 Lakini Sisera akakimbia kwa miguu, akaifikilia hema ya Yaeli mkewe Heberi, Mkeni; kwa maana palikuwa na amani kati ya Yabini, mfalme wa Hazori, na nyumba ya Heberi, Mkeni. 18 Yaeli akatoka kwenda kumlaki Sisera, akamwambia, Karibu Bwana wangu, karibu kwangu; usiogope. Akakaribia kwake hemani, naye akamfunika kwa bushuti. 19 Akamwambia, Tafadhali nipe maji kidogo ninywe; maana nina kiu. Akafungua chupa ya maziwa, akampa kunywa, akamfunika. 20 Naye akamwambia, Simama mlangoni pa hema; kisha itakuwa mtu awaye yote akija na kukuuliza, akisema, Je! Yupo mtu hapa, basi, mjibu, La, hapana. 21 Ndipo Yaeli, mkewe Heberi, akatwaa kigingi cha hema, akashika nyundo mkononi mwake, akamwendea polepole, akamtia kile kigingi katika kipaji chake, nacho kikapenya, hata kuingia mchangani; kwa maana usingizi mzito ulikuwa umemshika; basi akazimia, akafa. 22 Na tazama, Baraka alipokuwa akimfuatia Sisera; Yaeli akatoka ili kumlaki, akamwambia, Njoo, nami nitakuonyesha yule mtu unayemtafuta. Basi akamwendea, na tazama, Sisera amelala humo, amekufa, na hicho kigingi kilikuwa kipajini mwake. 23 Basi hivyo Mungu akamshinda Yabini, mfalme wa Kanaani mbele ya wana wa Israeli siku hiyo. 24 Mkono wa wana wa Israeli ukazidi kupata nguvu juu ya Yabini, mfalme wa Kanaani, hata walipokuwa wamemwangamiza Yabini, mfalme wa Kanaani.

Waamuzi 5

1 Ndipo Debora, na Baraka mwana wa Abinoamu, wakaimba siku ile, wakisema; 2 Kwa sababu wakuu walitangulia katika Israeli, Kwa sababu watu walijitoa nafsi zao kwa hiari yao, Mhimidini Bwana. 3 Sikieni, enyi wafalme; tegeni masikio, enyi wakuu; Mimi, naam mimi, nitamwimbia Bwana; Nitamhimidi Bwana, Mungu wa Israeli. 4 Bwana, ulipotoka katika Seiri, Ulipokwenda vitani kutoka mashamba ya Edomu, Nchi ilitetema, mbingu nazo zikadondoza maji, Naam, mawingu yakadondoza maji. 5 Milima ikayeyuka mbele za uso wa Bwana, Naam hata Sinai ule mbele za uso wa Bwana, Mungu wa Israeli. 6 Katika siku za Shamgari, mwana wa Anathi, Siku za Yaeli, njia kuu zilikuwa hazina watu; Nao wenye kusafiri walipita kwa njia za kando. 7 Maliwali walikoma katika Israeli, walikoma, Hata mimi Debora nilipoinuka, Nilipoinuka mimi, mama katika Israeli. 8 Walichagua miungu mipya, Ndipo kulikuwa na vita malangoni; Je! Ilionekana ngao au mkuki Katika watu elfu arobaini wa Israeli? 9 Moyo wangu unawaelekea maliwali wa Israeli, Waliojitoa nafsi zao kwa hiari yao miongoni mwa watu; Mhimidini Bwana. 10 Itangazeni habari, ninyi mpandao punda weupe, Ninyi mketio juu ya mazulia ya thamani, Na ninyi mnaopita njiani kwa miguu. 11 Mbali na kelele za hao wapigao mishale, katika mahali pa kuteka maji, Hapo watatangaza matendo ya haki ya Bwana; Naam, matendo ya haki ya kutawala kwake katika Israeli. Ndipo watu wa Bwana waliposhuka malangoni. 12 Amka, amka, Debora; Amka, amka, imba wimbo. Inuka, Baraka, wachukue mateka wao Waliokuchukua mateka, Ee mwana wa Abinoamu. 13 Ndipo walitelemka mabaki ya waungwana na ya watu; Bwana alishuka kwa ajili yangu apigane na mashujaa. 14 Kutoka Efraimu walitelemka wao ambao shina lao ni katika Amaleki, Nyuma yako, Benyamini, kati ya watu wako. Kutoka Makiri walishuka maliwali, Na kutoka Zabuloni wao washikao fimbo ya mwandishi. 15 Na wakuu wa Isakari walikuwa pamoja na Debora. Kama alivyokuwa Isakari, ndivyo alivyokuwa Baraka. Waliingia bondeni kwa kasi miguuni pake. Kwenye vijito vya Reubeni Palikuwa na makusudi makuu mioyoni. 16 Mbona ulikaa katika mazizi ya kondoo, Kusikiliza filimbi zipigwazo ili kuita makundi? Kwenye vijito vya Reubeni Palikuwa na makusudi makuu mioyoni. 17 Gileadi alikaa ng'ambo ya Yordani, Na Dani, mbona alikaa katika merikebu? Asheri alikaa kimya penye bandari ya bahari, Alikaa katika hori zake. 18 Zabuloni ndio watu waliohatirisha roho zao hata kufa; Nao Naftali mahali palipoinuka kondeni. 19 Wafalme walikuja wakafanya vita, Ndipo wafalme wa Kanaani walifanya vita. Katika Taanaki, karibu na maji ya Megido; Hawakupata faida yo yote ya fedha. 20 Walipigana kutoka mbinguni, Nyota katika miendo yao zilipigana na Sisera. 21 Mto ule wa Kishoni uliwachukua, Ule mto wa zamani, mto wa Kishoni. Ee roho yangu, endelea mbele kwa nguvu. 22 Ndipo kwato za farasi zilikanyaga-kanyaga Kwa sababu ya kupara-para, Kupara-para kwao wenye nguvu. 23 Ulaanini Merozi, alisema malaika wa Bwana, Walaanini kwa uchungu wenyeji wake; Kwa maana hawakuja kumsaidia Bwana, Kumsaidia Bwana juu ya hao wenye nguvu. 24 Atabarikiwa Yaeli kuliko wanawake wote; Mkewe Heberi, Mkeni, Atabarikiwa kuliko wanawake wote hemani. 25 Aliomba maji, naye akampa maziwa. Akamletea siagi katika sahani ya heshima. 26 Akanyosha mkono wake akashika kigingi, Nao mkono wake wa kuume ukashika nyundo ya fundi; Akampiga Sisera kwa hiyo nyundo, akamtoboa kichwa chake. Naam, alimpiga akamtoboa kipaji chake. 27 Miguuni pake aliinama, akaanguka, akalala. Miguuni pake aliinama, akaanguka. Hapo alipoinama, ndipo alipoanguka amekufa. 28 Alichungulia dirishani, akalia, Mama yake Sisera alilia dirishani; Mbona gari lake linakawia kufika? Mbona gurudumu za gari lake zinakawia? 29 Mabibi yake wenye akili wakamjibu, Naam, alijipa nafsi yake jawabu. 30 Je! Hawakupata mateka na kuyagawanya, Kijakazi, vijakazi wawili, kwa kila mtu? Kwa Sisera nyara ya mavazi ya rangi mbali mbali, Nyara za mavazi ya rangi mbali mbali ya darizi; Ya rangi mbali mbali ya darizi, pande zote mbili, Juu ya shingo za hao mateka. 31 Na waangamie vivyo hivyo adui zako wote, Ee Bwana.

Waamuzi 6

1 Kisha wana wa Israeli walifanya yaliyo maovu mbele za macho ya Bwana; Bwana akawatia mikononi mwa Midiani muda wa miaka saba 2 Mkono wa Midiani ulikuwa na nguvu juu ya Israeli; tena kwa sababu ya Midiani wana wa Israeli walijifanyia hayo mashimo yaliyo milimani, na hayo mapango, na hizo ngome. 3 Basi ikawa, hapo Israeli walipokuwa wamepanda mashamba, Wamidiani wakakwea, na Waamaleki, na hao wana wa mashariki; wakakwea juu yao; 4 wakapanga marago juu yao, na kuyaharibu hayo maongeo ya nchi, hata ufikapo Gaza, wala hawakuacha katika Israeli riziki ziwazo zote; kondoo, wala ng'ombe, wala punda. 5 Kwa maana walikwea na ng'ombe zao na hema zao, wakaja mfano wa nzige kwa wingi; wao na ngamia zao pia walikuwa hawana hesabu; nao waliingia katika hiyo nchi ili kuiharibu. 6 Israeli walitwezwa sana kwa sababu ya Wamidiani; nao wana wa Israeli wakamlilia Bwana. 7 Kisha ikawa, hapo wana wa Israeli walipomlilia Bwana kwa sababu ya Midiani, 8 Bwana akamtuma nabii aende kwa hao wana wa Israeli; naye akawaambia, Bwana, yeye Mungu wa Israeli, asema hivi, Mimi niliwaleta ninyi mkwee kutoka Misri, nikawatoa katika nyumba ya utumwa; 9 nami niliwaokoa na mikono ya Wamisri, na mikono ya wote waliokuwa wakiwaonea, nami niliwafukuza watoke mbele zenu, nami niliwapa ninyi nchi yao; 10 kisha niliwaambia, Mimi ndimi Bwana, Mungu wenu; msiiche miungu ya Waamori, ambayo mwaketi katika nchi yao; lakini hamkuitii sauti yangu. 11 Malaika wa Bwana akaenda akaketi chini ya mwaloni uliokuwa katika Ofra, uliokuwa mali yake Yoashi, Mwabiezeri; na mwanawe Gideoni alikuwa akipepeta ngano ndani ya shinikizo, ili kuificha machoni pa Wamidiani. 12 Malaika wa Bwana akamtokea, akamwambia, Bwana yu pamoja nawe, Ee shujaa. 13 Gideoni akamwambia, Ee Bwana wangu, ikiwa Bwana yu pamoja nasi, mbona mambo haya yote yametupata? Yako wapi matendo yake ya ajabu, waliyotuhadithia baba zetu, wakisema, Je! Siye Bwana, aliyetuleta huku kutoka Misri? Ila sasa ametutupa, naye ametutia katika mikono ya Midiani. 14 Bwana akamtazama, akasema, Enenda kwa uwezo wako huu, ukawaokoe Israeli na mkono wa Midiani. Je! Si mimi ninayekutuma? 15 Akamwambia, Ee Bwana, nitawaokoa Israeli kwa jinsi gani? Tazama, jamaa zangu ndio walio maskini sana katika Manase, na mimi ndimi niliye mdogo katika nyumba ya baba yangu. 16 Bwana akamwambia, Hakika nitakuwa pamoja nawe, nawe utawapiga Wamidiani kama mtu mmoja. 17 Naye akamwambia, Kama nimepata kibali mbele za macho yako, basi unionyeshe ishara, ya kuwa ndiwe wewe unayesema nami. 18 Tafadhali, usiondoke hapa hata nikujie, nikatoe zawadi yangu, na kuiweka mbele zako. Akasema, Nitangoja hata utakaporudi. 19 Basi Gideoni akaingia ndani, akaandaa mwana-mbuzi, na mikate isiyotiwa chachu, ya efa ya unga; akaitia ile nyama katika kikapu, akautia mchuzi katika nyungu, akamletea hapo nje chini ya mwaloni, akampa. 20 Naye malaika wa Mungu akamwambia, Itwae nyama na mikate isiyotiwa chachu, uiweke juu ya mwamba huu, ukaumwage huu mchuzi. Akafanya hivyo. 21 Ndipo malaika wa Bwana akanyosha ncha ya fimbo ile iliyokuwa mkononi mwake, akaigusa ile nyama na ile mikate; moto ukatoka mwambani, ukaiteketeza ile nyama na mikate; malaika wa Bwana akaondoka mbele ya macho yake. 22 Gideoni akaona ya kuwa ni malaika wa Bwana; Gideoni akasema, Ole wangu, Ee Bwana MUNGU! Kwa kuwa nimemwona Bwana uso kwa uso. 23 Bwana akamwambia Amani iwe pamoja nawe; usiogope; hutakufa. 24 Ndipo Gideoni akamjengea Bwana madhabahu hapo, akaiita jina lake, Yehova-Shalomu; hata hivi leo iko huko katika Ofra ya Waabiezeri. 25 Ikawa usiku uo huo Bwana akamwambia, Mtwae ng'ombe wa baba yako, yaani ng'ombe wa pili, wa miaka saba, ukaiangushe madhabahu ya Baali, aliyo nayo baba yako, ukaikate Ashera ile iliyo karibu nayo; 26 ukamjengee Bwana, Mungu wako, madhabahu juu ya ngome hii, kwa taratibu zake; ukamtwae yule ng'ombe wa pili na kumtoa awe sadaka ya kuteketezwa, kwa kuni za ile Ashera uliyoikata. 27 Ndipo Gideoni akatwaa watu kumi miongoni mwa watumishi wake, akafanya kama Bwana alivyomwambia; lakini ikawa kwa sababu aliwaogopa watu wa nyumba ya baba yake, na watu wa mji, hakuweza kuyatenda hayo wakati wa mchana, basi aliyatenda usiku. 28 Hata watu wa mji walipoondoka asubuhi na mapema, tazama, madhabahu ya Baali imebomolewa, na ile Ashera iliyokuwa karibu nayo imekatwa, na yule ng'ombe wa pili ametolewa sadaka juu ya ile madhabahu iliyojengwa. 29 Wakaambiana, Ni nani aliyetenda jambo hili? Hata walipotafuta habari na kuuliza, wakasema, Gideoni, mwana wa Yoashi, ndiye aliyetenda jambo hili. 30 Ndipo watu wa mji wakamwambia Yoashi Mlete mwanao, afe; kwa sababu ameibomoa madhabahu ya Baali na kwa sababu ameikata ile Ashera iliyokuwa karibu nayo. 31 Yoashi akawaambia watu wote waliokuwa wakishindana naye, Je! Mtamtetea Baali? Au mtamwokoa ninyi? Yeye atakayemtetea na auawe hivi asubuhi; kama yeye ni Mungu, na ajitetee nafsi yake, kwa sababu mtu mmoja ameibomoa madhabahu yake. 32 Basi akamwita Yerubaali siku hiyo, akisema, Baali na atete naye kwa ajili ya nafsi yake, kwa sababu ameibomoa madhabahu yake. 33 Wakati huo Wamidiani na Waamaleki, na hao wana wa mashariki walikutana pamoja; wakavuka na kupanga hema zao katika bonde la Yezreeli. 34 Lakini roho ya Bwana ikaja juu yake Gideoni; naye akapiga tarumbeta; na Abiezeri walikutanika na kumfuata. 35 Kisha akatuma wajumbe waende kati ya Manase yote; wao nao walikutana pamoja ili kumfuata; kisha akatuma wajumbe waende kwa Asheri, na kwa Zabuloni, na kwa Naftali; nao wakakwea ili kumlaki. 36 Gideoni akamwambia Mungu, Ikiwa wewe utawaokoa Israeli kwa mkono wangu, kama ulivyosema, 37 tazama, nitaweka ngozi ya kondoo katika kiwanja cha kupuria; na kama ukiwapo umande juu ya ngozi tu, na nchi yote ikiwa kavu, basi, hapo ndipo nitakapojua ya kuwa utawaokoa Israeli kwa mkono wangu, kama ulivyosema. 38 Ikawa hivyo; kwa maana aliondoka asubuhi na mapema, akaikamua ile ngozi, akautoa ule umande katika ile ngozi, bakuli zima la maji. 39 Gideoni akamwambia Mungu, Hasira yako isiwake juu yangu, nami nitasema mara hii tu; nakuomba, nijaribu kwa ngozi hii mara hii tu; sasa ngozi tu na iwe kavu, na uwe umande juu ya nchi yote. 40 Mungu akafanya hivyo usiku ule; maana ile ngozi tu ilikuwa kavu, napo palikuwa na umande juu ya nchi yote.

Waamuzi 7

1 Kisha Yerubaali, yaani Gideoni, na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka na mapema, wakapiga kambi yao karibu na kijito cha Harodi; na kambi ya Midiani ilikuwa upande wao wa kaskazini, karibu na mlima wa More, bondeni. 2 Bwana akamwambia Gideoni, Watu hawa walio pamoja nawe ni wengi mno hata nikawatie Wamidiani katika mikono yao, wasije Israeli wakajivuna juu yangu wakisema, Mkono wangu mwenyewe ndio ulioniokoa. 3 Basi sasa enda, tangaza habari masikioni mwa watu hawa, na kusema, Mtu awaye yote anayeogopa na kutetemeka, na arudi aondoke katika mlima wa Gileadi. Ndipo watu ishirini na mbili elfu wakarudi katika watu hao, wakabaki watu elfu kumi. 4 Bwana akamwambia Gideoni; Hata sasa watu hawa ni wengi mno; uwalete chini majini, nami nitawajaribu huko kwa ajili yako; kisha itakuwa ya kwamba yule nitakayekuambia, Huyu atakwenda pamoja nawe, ndiye atakayekwenda pamoja nawe; na mtu yule nitakayekuambia, Huyu hatakwenda pamoja nawe, basi mtu huyo hatakwenda. 5 Basi akawaleta watu chini majini. Bwana akamwambia Gideoni, Kila mtu atakayeyaramba maji kwa ulimi wake, kama vile arambavyo mbwa, huyo utamweka kando; kadhalika kila mtu apigaye magoti kunywa. 6 Na hesabu ya hao waliokunywa kwa kuramba-ramba, wakipeleka mkono kinywani, ilikuwa watu mia tatu; bali watu wengine wote walipiga magoti kunywa maji. 7 Bwana akamwambia Gideoni, Kwa watu hawa mia tatu walioyaramba maji nitawaokoa, nami nitawatia Wamidiani katika mikono yako; lakini watu hawa wote wengine na waende zao, kila mtu mahali pake. 8 Basi wale watu wakachukua vyakula vyao mikononi mwao, na tarumbeta zao; naye akawapeleka watu wote wa Israeli, kila mtu hemani kwake; bali aliwazuia wale watu mia tatu; na kambi ya Wamidiani ilikuwa chini yake, bondeni. 9 Ikawa usiku uo huo Bwana akamwambia, Ondoka, shuka kambini; maana nimeitia katika mikono yako. 10 Lakini, ukiogopa kushuka, shuka pamoja na Pura mtumishi wako kambini; 11 nawe utasikia wanayoyasema, na baada ya haya mikono yako itatiwa nguvu; ushuke kambini. Ndipo akashuka pamoja na Pura mtumishi wake hata kufikilia mwisho wa watu wenye silaha waliokuwa kambini. 12 Nao Wamidiani na Waamaleki na, hao wana wa mashariki walikuwa wametua bondeni, mfano wa nzige kwa wingi; na ngamia zao walikuwa hawana hesabu; mfano wa mchanga wa ufuoni, kwa wingi. 13 Hata Gideoni alipofika, tazama, palikuwa na mtu mmoja aliyekuwa akimhadithia mwenziwe ndoto, akasema, Tazama, naliota ndoto, na tazama, mkate wa shayiri ulianguka katika kambi ya Wamidiani, ukafika hata hema moja, ukaipiga hata ikaanguka, nao ukaipindua, hata ikalala chini. 14 Mwenzake akamjibu akasema, Habari hii haikosi kuwa upanga wa Gideoni, mwana wa Yoashi, mtu wa Israeli. Mungu amewatia Wamidiani na jeshi lote katika mkono wake. 15 Ikawa, aliposikia habari ya ile ndoto, na kufasiriwa kwake, akasujudu; akarudi katika jeshi la Israeli akasema, Inukeni, kwa maana Bwana amelitia jeshi la Midiani mikononi mwenu. 16 Kisha akawapanga wale watu mia tatu wawe vikosi vitatu, akatia tarumbeta katika mikono ya watu wote, na mitungi isiyo maji, na mienge ndani ya hiyo mitungi. 17 Akawaambia, Nitazameni, mkafanye kama nifanyavyo mimi; angalieni, nitakapofika mwisho wa kambi, itakuwa, nifanyavyo mimi nanyi fanyeni kadhalika. 18 Nitakapopiga tarumbeta, mimi na wote walio pamoja nami, basi ninyi nanyi zipigeni tarumbeta pande zote za kambi, mkaseme, Kwa Bwana, na kwa Gideoni. 19 Basi Gideoni, na wale watu mia waliokuwa pamoja naye, wakafika mwisho wa kambi, mwanzo wa zamu ya kati, wakati walipokuwa wamebadili wenye zamu; wakazipiga hizo tarumbeta, wakaivunja vipande vipande ile mitungi iliyokuwa mikononi mwao. 20 Vile vikosi vitatu wakapiga tarumbeta, wakaivunja mitungi, wakaishika mienge kwa mikono yao ya kushoto, na zile tarumbeta katika mikono yao ya kuume ili kuzipiga; wakapiga kelele, Upanga wa Bwana na wa Gideoni. 21 Wakasimama kila mtu mahali pake kuizunguka kambi pande zote; jeshi lote wakakimbia; nao wakapiga kelele, wakawakimbiza. 22 Wakazipiga zile tarumbeta mia tatu, naye Bwana akaufanya upanga wa kila mtu uwe juu ya mwenziwe, na juu ya jeshi lote, jeshi likakimbia mpaka Bethshita, kuendelea Serera, hata mpaka wa Abel-Mehola, karibu na Tabathi. 23 Wanaume wa Israeli walikuwa wamekusanyika kutoka Naftali, na kutoka Asheri, na kutoka Manase yote, wakawafuata Midiani. 24 Kisha Gideoni akapeleka wajumbe katika nchi yote ya vilima vilima ya Efraimu, akisema, Haya, telemkeni juu ya Midiani, na kuyashika hayo maji mbele yao, mpaka Bethbara, maana, huo mto wa Yordani. Basi watu waume wote wa Efraimu walikutana pamoja, wakayashika maji mpaka Bethbara, maana, huo mto wa Yordani. 25 Wakawashika hao wakuu wawili wa Midiani, Orebu na Zeebu; wakamwua huyo Orebu pale penye jabali la Orebu, na huyo Zeebu wakamwua hapo penye shinikizo la divai la Zeebu, kisha wakawaandamia Wamidiani; vichwa vya Orebu na Zeebu wakamletea Gideoni huko ng'ambo ya pili ya Yordani.

Waamuzi 8

1 Basi watu wa Efraimu wakamwambia, Kwa nini wewe kututendea sisi kama haya? Hata usituite, hapo ulipokwenda kupigana na Midiani? Nao wakateta naye sana. 2 Lakini akawaambia, Je! Mimi nimefanya nini sasa kama mlivyofanya ninyi? Hayo masazo ya zabibu za Efraimu si mema kuliko mavuno ya Abiezeri? 3 Mungu amewatia hao wakuu wa Midiani, Orebu na Zeebu, mikononi mwenu; na mimi nilipata kufanya nini kama mlivyofanya ninyi? Ndipo hasira zao walizokuwa nazo juu yake zikatulia aliposema maneno hayo. 4 Basi Gideoni akafika Yordani, akauvuka, yeye na hao watu mia tatu waliokuwa pamoja naye, walikuwa wamepungukiwa na nguvu, lakini wawafuatia vivyo. 5 Naye akawaambia watu wa Sukothi, Tafadhali wapeni mikate hao watu waniandamao; kwa maana wanapungukiwa na nguvu, nami ni katika kuwafuatia Zeba na Salmuna, wafalme wa Midiani. 6 Hao wakuu wa Sukothi wakasema, Je! Mikono ya Zeba na Salmuna i mkononi mwako sasa, hata sisi tukawape jeshi lako mikate? 7 Ndipo Gideoni akasema, Kwa sababu hii, hapo Bwana atakapokuwa amewatia Zeba na Salmuna mkononi mwangu, ndipo nitaipura nyama ya miili yenu kwa miiba ya nyikani, na kwa michongoma. 8 Basi kutoka hapo alikwea kwenda Penieli, akasema na watu wa mahali hapo maneno kama hayo; watu wa Penieli nao wakamjibu kama vile watu wa Sukothi walivyomjibu. 9 Naye akawaambia hao watu wa Penieli nao, akisema, Nitakapokuja tena kwa amani, nitauvunja mnara huu. 10 Basi hao kina Zebu na Salmuna walikuwa katika Karkori, na majeshi yao walikuwa pamoja nao, watu kama kumi na tano elfu hesabu yao, ni wote waliobaki wa hilo jeshi lote la hao wana wa mashariki; kwa sababu walianguka watu mia na ishirini elfu waliokuwa wenye kutumia upanga. 11 Basi Gideoni alikwea kwa njia ya hao waliokuwa wenye kukaa hemani upande wa mashariki wa Noba na Yogbeha, akalipiga hilo jeshi; kwa maana lile jeshi lilikuwa salama. 12 Zeba na Salmuna walikimbia; naye akawaandamia; akawakamata hao wafalme wawili wa Midiani Zeba na Salmuna, akalitapanya-tapanya hilo jeshi lote. 13 Kisha huyo Gideoni mwana wa Yoashi akarudi kutoka vitani, kutoka kwenye makweleo ya Heresi. 14 Ndipo akamshika mtu mmoja hirimu katika watu wa Sukothi, akamwuliza; naye akamwandikia majina ya hao wakuu wa Sukothi, na wazee wa mji, watu sabini na saba. 15 Kisha akawafikilia wale watu wa Sukothi, akawaambia, Tazama, Zeba na Salmuna, ambao ninyi mlinisimanga kwa ajili yao, mliposema, Je! Mikono ya Zeba na Salmuna iko sasa mikononi mwako wewe, hata tuwape watu wako waliochoka mikate? 16 Basi akawatwaa hao wazee wa mji, na miiba ya nyikani na michongoma, akawafunza hao watu wa Sukothi kwayo. 17 Kisha akaupomosha mnara wa Penieli, na kuwaua watu wa mji huo. 18 Ndipo akawaambia hao Zeba na Salmuna, Hao watu mliowaua huko Tabori walikuwa watu wa namna gani? Wakamjibu, Walikuwa kama wewe ulivyo; kila mmoja alikuwa anafanana na wana wa mfalme. 19 Naye akasema, Watu hao walikuwa ndugu zangu, wana wa mamaangu mimi; kama yeye Bwana alivyo hai, kwamba mliwaokoa hai watu hao, mimi nisingewaua ninyi. 20 Kisha akamwambia Yetheri mwanawe mzaliwa wa kwanza, Haya, simama, uwaue hawa. Lakini huyo kijana hakutoa upanga wake; maana, akacha, kwa sababu alikuwa ni kijana tu. 21 Ndipo hapo Zeba na Salmuna wakasema, Simama wewe ukatuangukie sisi; kwa maana kama mtu alivyo, ndivyo zilivyo nguvu zake. Basi Gideoni akasimama, akawaua Zeba na Salmuna, akazitwaa koja zilizokuwa katika shingo za ngamia zao. 22 Ndipo watu wa Israeli wakamwambia Gideoni, Tawala wewe juu yetu, wewe, na mwanao, na mjukuu wako pia; kwa kuwa wewe umetuokoa na mikono ya Midiani. 23 Gideoni akawaambia, Mimi sitatawala juu yenu wala mwanangu hatatawala juu yenu; yeye Bwana atatawala juu yenu. 24 Kisha Gideoni akawaambia, Mimi nina haja yangu niitakayo kwenu, ni ya kila mtu kunipa hizo pete za masikio ya mateka yake. (Kwa maana walikuwa na pete za masikio za dhahabu, kwa sababu walikuwa ni Waishmaeli.) 25 Wakajibu, Tutakupa kwa mioyo. Basi wakatandika nguo chini, wakatia humo kila mtu pete za masikio ya mateka yake. 26 Na uzani wa hizo pete za dhahabu alizozitaka ulipata shekeli za dhahabu elfu moja na mia saba; mbali na makoja na vidani, na mavazi ya rangi ya zambarau waliyokuwa wameyavaa hao wafalme wa Midiani, tena mbali na mikufu iliyokuwa katika shingo za ngamia zao. 27 Basi Gideoni akafanya naivera kwa vitu vile, akaiweka katika mji wake, mji huo wa Ofra; nao Israeli wote wakaenda na kuiandama kwa ukahaba huko; nayo ilikuwa ni tanzi kwa Gideoni na kwa nyumba yake. 28 Hivyo Midiani walishindwa mbele ya wana wa Israeli, wala hawakuinua vichwa vyao tena. Nayo nchi ilipata kuwa na amani muda wa miaka arobaini katika siku za Gideoni. 29 Kisha huyo Yerubaali, mwana wa Yoashi, akaenda kukaa katika nyumba yake mwenyewe. 30 Gideoni alikuwa na wana sabini waliozawa na mwili wake; kwa maana alikuwa na wake wengi. 31 Na suria yake aliyekuwako Shekemu, yeye naye akamzalia mwana, naye akamwita jina lake Abimeleki. 32 Basi Gideoni mwana wa Yoashi akafa mwenye umri wa uzee mwema, akazikwa katika kaburi la Yoashi baba yake, katika Ofra ya Waabiezeri. 33 Kisha ikawa, mara alipokufa Gideoni, wana wa Israeli wakakengeuka tena, wakawaandama Mabaali kwa ukahaba, wakamfanya Baal-berithi kuwa ni mungu wao. 34 Kwani wana wa Israeli hawakumkumbuka Bwana, Mungu wao, ambaye ndiye aliyewaokoa na mikono ya adui zao wote pande zote; 35 wala hawakuifanyia mema nyumba ya Yerubaali, yaani Gideoni, kwa kuyafuata hayo mema yote aliyowafanyia Israeli.

Waamuzi 9

1 Abimeleki, mwana wa Yerubaali, akaenda Shekemu kwa ndugu za mama yake, akanena nao, na wote waliokuwa wa nyumba ya baba ya mama yake, akasema, 2 Haya, neneni tafadhali masikioni mwa waume wote wa Shekemu, mkaulize, Je! Ni lipi lililo jema kwenu, kwamba hao wana wa Yerubaali wote, ambao ni watu sabini, watawale juu yenu, au kwamba mtu mmoja atawale juu yenu? Tena kumbukeni ya kwamba mimi ni mfupa na nyama yenu. 3 Hao ndugu za mama yake wakanena habari zake masikioni mwa hao watu wote wa Shekemu maneno hayo yote; na mioyo yao ikaelekea kumwandama Abimeleki; kwa kuwa walisema, Huyu ni ndugu yetu. 4 Wakampa vipande vya fedha sabini vilivyotoka katika nyumba ya Baal-berithi, na kwa fedha hizo Abimeleki akaajiri watu wapuuzi mabaradhuli, wafuatane naye. 5 Kisha akaenda nyumbani kwa babaye huko Ofra, akawaua nduguze, hao wana wa Yerubaali, watu sabini, akawaua juu ya jiwe moja; lakini Yothamu, mwana mdogo wa Yerubaali, alisalia; kwa maana alijificha. 6 Kisha hao watu wote wa Shekemu wakakusanyika pamoja, na jamaa yote ya Milo, wakaenda na kumtawaza Abimeleki awe mfalme, karibu na huo mgandi ulio karibu na ngome iliyo katika Shekemu. 7 Kisha walipomwambia huyo Yothamu, yeye akaenda, akasimama juu ya kilele cha kilima cha Gerizimu, akapaza sauti yake, akapiga kelele, na kuwaambia, Nisikieni mimi, enyi watu wa Shekemu, ili kwamba Mungu naye apate kuwasikia ninyi. 8 Siku moja miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao; ikauambia mti mzeituni, Tawala wewe juu yetu. 9 Lakini huo mzeituni ukaiambia, Je! Niache mafuta yangu, ambayo kwangu mimi watu wamheshimu Mungu na wanadamu, ili niende nikayonge-yonge juu ya miti? 10 Kisha miti ikauambia mtini, Njoo wewe, utawale juu yetu. 11 Lakini huo mtini ukaiambia, Je! Niuache utamu wangu, na matunda yangu mazuri, niende nikayonge-yonge juu ya miti? 12 Kisha miti ikauambia mzabibu, Njoo wewe, utawale juu yetu. 13 Huo mzabibu nao ukaiambia, Je! Niiache divai yangu, ambayo humfurahisha Mungu na wanadamu, ili niende nikayonge-yonge juu ya miti? 14 Ndipo hiyo miti yote ikauambia mti wa miiba, Njoo wewe, utawale juu yetu. 15 Huo mti wa miiba ukaiambia miti, Kwamba ninyi mwanitia mafuta niwe mfalme juu yenu kwelikweli, basi njoni mtumaini kivuli changu; na kwamba sivyo, na utoke moto katika mti wa miiba na kuiteketeza mierezi ya Lebanoni. 16 Basi sasa ikiwa mmetenda kwa uaminifu na uelekevu, katika kumtawaza Abimeleki awe mfalme, na ikiwa mmemtendea mema Yerubaali na nyumba yake, na kumtendea kama ilivyostahili mikono yake; 17 (kwa maana baba yangu aliwatetea ninyi, na kuhatirisha uhai wake, na kuwaokoa na mikono ya Midiani; 18 nanyi mmeinuka juu ya nyumba ya baba yangu hivi leo nanyi mmewaua wanawe, watu sabini, juu ya jiwe moja, nanyi mmemtawaza Abimeleki, mwana wa kijakazi chake, awe mfalme juu ya watu wa Shekemu kwa sababu yeye ni ndugu yenu;) 19 basi ikiwa mmemtendea kwa uaminifu na uelekevu Yerubaali na nyumba yake hivi leo, basi furahini ninyi katika huyo Abimeleki, yeye naye na afurahi kwenu ninyi; 20 lakini kwamba sivyo hivyo, basi, moto na utoke katika Abimeleki na kuwateketeza watu wa Shekemu, na jamaa ya Milo; kisha moto na utoke katika hao watu wa Shekemu, na katika jamaa ya Milo, na kumteketeza Abimeleki. 21 Kisha Yothamu akaenda zake na kukimbia, akaenda Beeri, na kukaa kuko, kwa kumwogopa Abimeleki nduguye. 22 Basi Abimeleki alitawala juu ya Israeli muda wa miaka mitatu. 23 Kisha Mungu akapeleka roho mbaya kati ya Abimeleki na watu wa Shekemu; nao watu wa Shekemu wakamtendea Abimeleki kwa udanganyifu; 24 ili kwamba huo udhalimu waliotendewa hao wana sabini wa Yerubaali uje, tena kwamba damu yao iandikwe juu ya Abimeleki ndugu yao, aliyewaua, na juu ya watu wa Shekemu, waliomtia nguvu mikono yake ili awaue hao nduguze. 25 Basi watu wa Shekemu wakaweka watu kumvizia juu ya vilele vya milima, ambao waliwanyang'anya vitu vyao watu wote waliopita njia hiyo karibu nao; naye Abimeleki aliambiwa. 26 Kisha Gaali, mwana wa Ebedi, akaenda pamoja na nduguze, wakavuka na kufika Shekemu; na watu wa Shekemu wakamtumaini yeye. 27 Nao wakatoka kwenda mashambani, wakavuna mashamba yao ya mizabibu, na kuzishindika hizo zabibu, na kufanya sikukuu, kisha wakaingia nyumbani mwa mungu wao, wakala na kunywa na kumlaani huyo Abimeleki. 28 Naye Gaali mwana wa Ebedi akasema, Abimeleki ni nani, na Shekemu ni nani, hata tukamtumikie yeye? Yeye, je! Si mwana wa Yerubaali? Na Zebuli siye akida wake? Haya, ninyi watumikieni hao watu wa Hamori, babaye Shekemu; Lakini sisi je! Tumtumikie kwa sababu gani? 29 Laiti watu hawa wangekuwa chini ya mkono wangu! Hapo basi mimi ningemwondoa huyo Abimeleki. Kisha akamwambia Abimeleki, Haya, ongeza askari zako, utoke nje. 30 Basi hapo Zebuli, aliyekuwa liwali wa mji, alipoyasikia hayo maneno ya Gaali mwana wa Ebedi, hasira zake zikamwaka. 31 Naye akatuma wajumbe waende kwa Abimeleki kwa siri, akasema, Tazama, Gaali, mwana wa Ebedi, na ndugu zake wamekuja Shekemu; na tazama waufitinisha mji huu kinyume chako. 32 Basi sasa, inuka wewe, usiku, wewe na watu walio pamoja nawe, mvizie mashambani; 33 kisha itakuwa, asubuhi, mara litakapokucha jua, wewe utaamka asubuhi na mapema, na kuushambulia mji huo; tena, angalia, hapo yeye na wale watu walio pamoja naye watakapokutokea nje kupigana nawe, ndipo utapata kuwatenda kama utakavyopata nafasi. 34 Basi Abimeleki akainuka na watu wote waliokuwa pamoja naye, usiku nao wakauvizia Shekemu kwa vikosi vinne. 35 Huyo Gaali mwana wa Ebedi akatoka nje, akasimama penye maingilio ya lango la mji; naye Abimeleki na hao watu waliokuwa pamoja naye wakainuka kutoka mahali pale walipokuwa wanavizia. 36 Basi Gaali alipowaona hao watu, akamwambia Zebuli, Tazama, watu washuka kutoka katika vilele vya milima. Zebuli akamwambia, Ni kivuli cha milima unachokiona kama ndio watu. 37 Kisha Gaali akasema mara ya pili, akanena, Angalia, watu washuka katikati ya nchi, na kikosi kimoja kinakuja kwa njia ya mwaloni wa Meonenimu. 38 Ndipo Zebuli akamwambia, Je! Kinywa chako sasa ki wapi, hata ukasema Huyo Abimeleki ni nani, hata inatupasa kumtumikia yeye? Je! Hawa sio watu hao uliowadharau wewe? Haya, toka nje sasa, tafadhali, upigane nao. 39 Basi Gaali akatoka nje mbele ya watu wa Shekemu, akapigana na Abimeleki. 40 Lakini Abimeleki akamkimbiza, naye akakimbia mbele yake, wengi wakaanguka waliojeruhiwa hata kufikilia maingilio ya hilo lango. 41 Abimeleki akakaa Aruma; naye Zebuli akawatoa Gaali na ndugu zake, wasikae katika Shekemu. 42 Ikawa siku ya pili yake, watu wakatoka waende mashambani; naye Abimeleki aliambiwa. 43 Naye akawatwaa watu wake, na kuwagawanya wawe vikosi vitatu, nao wakavizia mashambani; naye akaangalia, na tazama, watu walikuwa watoka humo mjini; basi akainuka na kupigana nao, akawapiga. 44 Abimeleki, na vile vikosi vilivyokuwa pamoja naye, wakafuliza kwenda mbele, wakasimama penye maingilio ya lango la mji, na vile vikosi viwili vikawarukia hao wote waliokuwa mashambani, na kuwapiga. 45 Abimeleki akapigana na huo mji mchana kutwa; akautwaa mji, akawaua watu waliokuwamo ndani yake; kisha akaupomosha mji, na kuutia chumvi. 46 Kisha watu wote waliokaa katika ile buruji ya Shekemu waliposikia habari hiyo wakaingia ndani ya ngome ya nyumba ya El-berithi. 47 Abimeleki aliambiwa ya kuwa watu hao wote wa buruji ya Shekemu wamekutana pamoja. 48 Basi Abimeleki akakwea kwenda kilima cha Salmoni, yeye na wote waliokuwa pamoja naye; naye Abimeleki akashika shoka mkononi mwake, akakata tawi moja katika miti, akalishika na kujitweka fuzini mwake; akawaambia hao watu waliokuwa pamoja naye, Haya, mliyoniona mimi kufanya, fanyeni upesi vivyo, kama nilivyofanya mimi. 49 Basi watu hao wote vivyo wakakata kila mtu tawi lake, wakamwandama Abimeleki, wakayaweka hayo matawi pale ngomeni, na kuiteketeza moto hiyo ngome juu yao; basi hivyo watu wote wa hiyo buruji ya Shekemu wakafa, walipata kama watu elfu, waume kwa wake. 50 Ndipo Abimeleki alipokwenda Thebesi, akapanga kinyume cha Thebesi na kuutwaa. 51 Lakini ndani ya huo mji palikuwa na buruji yenye nguvu, na watu wote waume na wake wakakimbilia huko, na watu wote wa mji, nao wakajifungia ndani, wakapanda paa la buruji. 52 Abimeleki akaiendea hiyo buruji na kupigana nayo; naye akaukaribia mlango wa buruji ili auteketeze kwa moto. 53 Na mwanamke mmoja akabwaga jiwe la kusagia la juu, nalo likampiga Abimeleki kichwani, na kulivunja fuvu la kichwa chake. 54 Ndipo akamwita kwa haraka huyo kijana aliyekuwa anamchukulia silaha zake, na kumwambia, Futa upanga wako, uniue, ili watu wasiseme juu yangu Aliuawa na mwanamke. Basi huyo kijana wake akamchoma upanga, naye akafa. 55 Basi hapo watu wa Israeli walipoona ya kuwa Abimeleki amekufa, wakaondoka wakaenda kila mtu mahali pake. 56 Basi hivyo Mungu akalipiza kisasi juu ya uovu wa Abimeleki aliomtenda baba yake, katika kuwaua hao nduguze watu sabini; 57 uovu wote wa watu wa Shekemu Mungu alilipiza juu ya vichwa vyao; na hiyo laana ya Yothamu mwana wa Yerubaali ikawajilia juu yao.

Waamuzi 10

1 Baada yake Abimeleki, akainuka Tola mwana wa Pua, mwana wa Dodo, mtu wa Isakari, kuwaokoa Israeli; naye alikuwa akikaa Shamiri, katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu. 2 Huyo akawa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka ishirini na mitatu, akafa, akazikwa katika Shamiri. 3 Baada yake huyo akainuka Yairi, Mgileadi; naye akawa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka ishirini na miwili. 4 Huyo alikuwa na wana thelathini waliokuwa wakipanda wana-punda thelathini, nao walikuwa na miji thelathini, ambayo inaitwa Hawoth-yairi hata hivi leo, nayo iko katika nchi ya Gileadi. 5 Yairi akafa, akazikwa huko Kamoni. 6 Kisha wana wa Israeli walifanya tena yaliyo maovu mbele za macho ya Bwana, wakawatumikia Mabaali, na Maashtorethi, na miungu ya Shamu, na miungu ya Sidoni, na miungu ya Moabu, na miungu ya wana wa Amoni, na miungu ya Wafilisti; nao wakamwacha Bwana, wala hawakumtumikia yeye. 7 Hasira za Bwana ziliwaka juu ya Israeli, akawauza na kuwaua mikononi mwa Wafilisti, na mikononi mwa wana wa Amoni. 8 Nao wakawasumbua na kuwaonea wana wa Israeli mwaka huo; waliwaonea wana wa Israeli wote waliokuwa ng'ambo ya pili ya Yordani katika nchi ya Waamori, iliyoko huko Gileadi, muda wa miaka kumi na minane. 9 Wana wa Amoni nao wakavuka Yordani ili wapigane na Yuda, na kupigana na Benyamini, na nyumba ya Efraimu; basi hivyo Israeli walikuwa wanasumbuliwa sana. 10 Ndipo wana wa Israeli wakamlilia Bwana, wakisema, Sisi tumekufanyia dhambi, kwa sababu tumemwacha Mungu wetu, na kuyatumikia Mabaali. 11 Naye Bwana akawaambia wana wa Israeli, Je! Sikuwaokoa ninyi na hao Wamisri, na Waamori, na wana wa Amoni, na Wafilisti? 12 Hao Wasidoni nao, na Waamaleki, na Wamaoni, waliwaonea, nanyi mlinililia, nami niliwaokoa na mikono yao. 13 Lakini mmeniacha mimi, na kuitumikia miungu mingine; basi kwa ajili ya hayo mimi sitawaokoa tena. 14 Haya, endeni mkaililie hiyo miungu mliyoichagua; na hiyo iwaokoe wakati wa kusumbuka kwenu. 15 Wana wa Israeli wakamwambia Bwana Tumefanya dhambi; utufanyie yote uyaonayo kuwa ni mema; lakini tuokoe, twakusihi, siku hii ya leo, haya tu. 16 Nao wakaiondoa hiyo miungu ya kigeni iliyokuwa kati yao, nao wakamtumikia Bwana; na roho yake ilihuzunika kwa sababu ya msiba wa Israeli. 17 Wakati huo wana wa Amoni walikutana pamoja, wakapanga marago huko Gileadi. Wana wa Israeli nao wakajikusanya wakapanga marago Mispa. 18 Na hao watu, wakuu wa Gileadi, wakaambiana wao kwa wao, Je! Ni mtu yupi atakayeanza kupigana na wana wa Amoni? Yeye atakuwa ni kichwa juu ya wenyeji wote wa Gileadi.

Waamuzi 11

1 Basi huyo Yeftha, Mgileadi, alikuwa mtu shujaa sana, naye alikuwa ni mwana wa mwanamke kahaba; Gileadi akamzaa Yeftha. 2 Mkewe huyo Gileadi akamzalia wana; na hao wana wa mkewe hapo walipokuwa wamekua wakubwa wakamtoa Yeftha, na kumwambia, Wewe hutarithi katika nyumba ya babaetu; kwa sababu wewe u mwana wa mwanamke mwingine. 3 Ndipo Yeftha akawakimbia hao nduguze, akakaa katika nchi ya Tobu; na watu mabaradhuli walikwenda na kutangamana na Yeftha, wakatoka kwenda pamoja naye. 4 Ikawa baadaye, wana wa Amoni wakapigana na Israeli. 5 Ikatukia, hapo wana wa Amoni walipopigana na Israeli, wazee wa Gileadi wakaenda kumtwaa huyo Yeftha katika ile nchi ya Tobu; 6 wakamwambia Yeftha, Njoo wewe uwe kichwa chetu, ili tupate kupigana na wana wa Amoni. 7 Yeftha akawaambia wazee wa Gileadi, Je! Ninyi hamkunichukia mimi na kunifukuza nitoke katika nyumba ya baba yangu? Basi kwani kunijilia hivi sasa wakati mlio katika taabu? 8 Wazee wa Gileadi wakamwambia Yeftha, Kwa ajili ya hayo sasa tumegeuka kukuelekea wewe tena, ili uende pamoja nasi na kupigana na wana wa Amoni, nawe utakuwa kichwa chetu juu ya wenyeji wote wa Gileadi. 9 Basi Yeftha akawaambia wazee wa Gileadi Kwamba mwanirejeza kwetu tena ili kupigana na wana wa Amoni, naye Bwana akiwatoa mbele yangu, je! Mimi nitakuwa kichwa chenu? 10 Wazee wa Gileadi wakamwambia Yeftha, Yeye Bwana atakuwa shahidi kati yetu; hakika yetu tutafanya sawasawa na neno lako. 11 Ndipo Yeftha akaenda pamoja na wazee wa Gileadi, na hao watu wakamfanya awe kichwa, tena mkuu, juu yao; naye Yeftha akanena maneno yake yote mbele ya Bwana huko Mispa. 12 Basi Yeftha akatuma wajumbe waende kwa mfalme wa wana wa Amoni akasema, Je! Wewe una nini nami, hata umenijilia kupigana juu ya nchi yangu? 13 Mfalme wa wana wa Amoni akawajibu hao wajumbe wa Yeftha Kwa sababu Israeli waliitwaa nchi yangu, hapo walipokwea kutoka katika nchi ya Misri, tokea Arnoni mpaka Yaboki, na hata Yordani; basi sasa rudisha hizo nchi tena pasipo matata. 14 Yeftha akatuma wajumbe mara ya pili waende kwa huyo mfalme wa wana wa Amoni; 15 akamwambia, Yeftha akuambia hivi; Israeli hakuitwaa nchi ya Moabu, wala nchi ya wana wa Amoni; 16 lakini hapo walipokwea kutoka Misri, na Israeli walienenda katika bara hata kuifikilia Bahari ya Shamu, na kufikilia Kadeshi; 17 ndipo Israeli wakatuma wajumbe waende kwa mfalme wa Edomu, wakisema, Nakuomba sana unipe ruhusa nipite katika nchi yako; lakini mfalme wa Edomu hakusikia. Ni vivyo wakampelekea wajumbe mfalme wa Moabu; wala yeye hakukubali; basi Israeli wakakaa katika Kadeshi. 18 Kisha akaenda nyikani na kuizunguka hiyo nchi ya Edomu, na nchi ya Moabu, nao wakapita upande wa mashariki wa nchi ya Moabu, wakapanga marago upande wa pili wa Arnoni; wala hawakuingia ndani ya mpaka wa Moabu, kwa maana Arnoni ilikuwa ni mpaka wa Moabu. 19 Kisha Israeli wakatuma wajumbe waende kwa Sihoni mfalme wa Waamori, mfalme wa Heshboni: Israeli wakamwambia, Twakuomba utupe ruhusa tupite katika nchi yako, mpaka mahali pangu. 20 Lakini huyo Sihoni hakuwaamini Israeli ili wapite ndani ya mpaka wake; bali Sihoni akawakutanisha watu wake wote, nao wakapanga kambi katika Yahasa, wakapigana na Israeli. 21 Bwana, Mungu wa Israeli, akamtia Sihoni na watu wake wote mikononi mwa Israeli, nao wakawapiga; basi Israeli wakaimiliki hiyo nchi ya Waamori, wenye kukaa nchi hiyo. 22 Nao wakaumiliki mpaka wote wa Waamori, tokea Arnoni hata Yaboki, tokea hiyo bara hata Yordani. 23 Basi sasa yeye Bwana, Mungu wa Israeli, amewapokonya Waamori watoke mbele ya watu wake Israeli, na wewe wataka kuwatamalaki? 24 Je! Wewe hutakitamalaki hicho ambacho huyo Kemoshi mungu wako akupa kukitamalaki? Kadhalika, awaye yote ambaye Bwana, Mungu wetu, amemfukuza atoke mbele yetu hao ndio tutakaowatamalaki. 25 Na wewe sasa, je! U mwema kuliko Balaki mwana wa Sipori, huyo mfalme wa Moabu, kwa lo lote? Je! Yeye alishindana na Israeli, au kupigana nao? 26 Wakati Israeli waliokuwa wakikaa Heshboni na miji yake, na katika Aroeri na miji yake, na katika miji hiyo yote iliyo huko kando ya Arnoni, muda wa miaka mia tatu; mbona ninyi hamkuipata tena katika majira hayo? 27 Basi mimi sikukufanyia wewe dhambi, lakini wewe unanitenda uovu kwa kupigana nami; yeye Bwana, yeye Mwamuzi, na awe mwamuzi hivi leo kati ya wana wa Israeli na wana wa Amoni. 28 Lakini mfalme wa wana wa Amoni hakuyasikiza hayo maneno ya Yeftha aliompelekea. 29 Ndipo roho ya Bwana ikamjilia juu yake Yeftha, naye akapita katika Gileadi na Manase, akapita na katika Mispa ya Gileadi, na kutoka hapo Mispa ya Gileadi akapita kuwaendea wana wa Amoni. 30 Naye Yeftha akamwekea Bwana nadhiri, akasema, Kwamba wewe utawatia wana wa Amoni mkononi mwangu kweli, 31 ndipo itakuwa ya kwamba, kile kitakachotoka katika milango ya nyumba yangu kunilaki, hapo nitakaporudi na amani kutoka kwa hao wana wa Amoni, kitu hicho kitakuwa ni cha Bwana, nami nitakisongeza kiwe sadaka ya kuteketezwa. 32 Basi Yeftha akavuka kuwaendea wana wa Amoni ili kupigana nao; naye Bwana akawaua mkononi mwake. 33 Akawapiga kutoka Aroeri hata kufikilia Minithi, miji ishirini, na mpaka Abel-keramimu, akawapiga kwa machinjo makuu mno. Basi hivyo wana wa Amoni walishindwa mbele ya wana wa Israeli. 34 Kisha Yeftha akafika Mispa nyumbani kwake, na tazama, binti yake akamtokea kumlaki, na matari na machezo; naye alikuwa ni mwanawe pekee; hakuwa na mwingine, mwana wala binti, ila yeye. 35 Ikawa alipomwona akayararua mavazi yake, akasema, Ole wangu! Mwanangu, umenitweza sana, nawe u mmoja miongoni mwa hao wanisumbuao; kwa kuwa mimi nimemfunulia Bwana kinywa changu, nami siwezi kurejea nyuma. 36 Binti yake akamwambia, Baba yangu, wewe umemfunulia Bwana kinywa chako; basi unifanyie sawasawa na hayo yaliyotoka kinywani mwako; kwa kuwa yeye Bwana amekulipia kisasi juu ya adui zako, hao wana wa Amoni. 37 Kisha akamwambia baba yake, Basi na nifanyiwe neno hili; niache peke yangu muda wa miezi miwili, ili nipate kwenenda milimani, na kuombolea uanawali wangu, mimi na wenzangu. 38 Akamwambia, Haya, enda. Akampeleka mbali muda wa miezi miwili; naye akaenda zake, yeye na wenziwe, akauombolea uanawali wake huko milimani. 39 Basi ikawa mwisho wa hiyo miezi miwili, akarudi kwa babaye, aliyemtenda sawasawa na ile nadhiri yake aliyokuwa ameiweka; naye alikuwa hajamjua mtu mume. Kisha ikawa desturi katika Israeli, 40 kwamba binti za Israeli waende mwaka baada ya mwaka ili kumkumbuka huyo mwana wa Yeftha, Mgileadi, siku nne katika mwaka.

Waamuzi 12

1 Kisha watu wa Efraimu walikutana pamoja na kupita kwenda upande wa kaskazini; wakamwambia Yeftha, Kwa nini wewe kuvuka kwenda kupigana na wana wa Amoni, nawe hukutuita sisi kwenda pamoja nawe? Tutaipiga moto nyumba yako juu yako. 2 Yeftha akawaambia, Mimi na watu wangu tulikuwa na matata makubwa na wana wa Amoni; nami hapo nilipowaita ninyi, hamkuniokoa na mikono yao. 3 Nami nilipoona ya kuwa ninyi hamniokoi, niliuhatirisha uhai wangu, na kuvuka ili nipigane na wana wa Amoni, Bwana naye akawatia mkononi mwangu; basi kwa nini ninyi kunijia hivi leo kutaka kupigana nami? 4 Ndipo Yeftha akawakutanisha watu wote wa Gileadi, na kupigana na Efraimu; na hao watu wa Gileadi wakawapiga Efraimu, kwa sababu walisema, Ninyi Wagileadi ni watoro mliotoroka Efraimu, mnaokaa kati ya Efraimu, na kati ya Manase. 5 Nao Wagileadi wakavishika vivuko vya Yordani kinyume cha hao Waefraimu; kisha ilikuwa, hapo watoro waliotoroka Efraimu mmojawapo aliposema Niache nivuke, hao watu wa Gileadi wakamwambia, Je! Wewe u Mwefraimu? Kwamba alisema, La; 6 ndipo wakamwambia, Haya, tamka sasa neno hili, Shibolethi; naye akasema, Sibolethi; kwa maana hakuweza kufanya midomo yake kutamka neno hilo sawasawa; ndipo wakamshika, na kumwua hapo penye vivuko vya Yordani; basi wakaanguka wakati huo watu arobaini na mbili elfu wa Efraimu. 7 Huyo Yeftha akawa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka sita. Ndipo akafa Yeftha, Mgileadi, akazikwa katika miji ya Gileadi mmojawapo. 8 Baada yake huyo, Ibzani wa Bethlehemu akawa mwamuzi wa Israeli. 9 Alikuwa na wana thelathini; na binti thelathini akawapeleka waende mahali pengine, kisha akaleta wanawake thelathini kutoka mahali pengine kwa ajili ya hao wanawe. Akawa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka saba. 10 Huyo Ibzani akafa, akazikwa huko Bethlehemu. 11 Baada yake huyo, Eloni, Mzabuloni, akawa mwamuzi wa Israeli akawaamua Israeli muda wa miaka kumi. 12 Huyo Eloni, Mzabuloni, akafa, akazikwa katika Aiyaloni katika nchi ya Zabuloni. 13 Baada yake huyo, Abdoni mwana wa Hileli, Mpirathoni, akawa mwamuzi wa Israeli. 14 Naye alikuwa na wana arobaini, na wajukuu thelathini, waliokuwa wakipanda wana-punda sabini; akawa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka minane. 15 Huyo Abdoni mwana wa Hileli, Mpirathoni, akafa, akazikwa huko Pirathoni katika nchi ya Efraimu, katika nchi ya vilima ya Waamaleki.

Waamuzi 13

1 Wana wa Israeli wakafanya tena yaliyo mabaya mbele za macho ya Bwana, Bwana akawatia katika mikono ya Wafilisti, muda wa miaka arobaini. 2 Palikuwa na mtu mmoja wa Sora, wa jamaa ya Wadani; jina lake akiitwa Manoa; na mkewe alikuwa tasa, hakuzaa watoto. 3 Malaika wa Bwana akamtokea yule mwanamke, akamwambia, Tazama, wewe sasa u tasa, huzai; lakini utachukua mimba, nawe utamzaa mtoto mwanamume. 4 Basi sasa, jihadhari, nakuomba, usinywe divai wala kileo, wala usile kitu kilicho najisi; 5 kwani tazama, utachukua mimba, nawe utamzaa mtoto mwanamume; na wembe usipite juu ya kichwa chake; maana mtoto huyo atakuwa mnadhiri wa Mungu tangu tumboni; naye ataanza kuwaokoa Israeli na mikono ya Wafilisti. 6 Ndipo yule mwanamke akaenda akamwambia mume wake, akisema, Mtu wa Mungu alinijia, na uso wake ulikuwa kama uso wa malaika wa Mungu, wa kutisha sana; nami sikumwuliza, Umetoka wapi? Wala hakuniambia jina lake; 7 lakini aliniambia, Tazama, utachukua mimba, nawe utamzaa mtoto mwanamume; basi sasa, usinywe divai wala kileo, wala usile kitu kilicho najisi. Maana mtoto huyo atakuwa Mnadhiri wa Mungu tangu tumboni, hata siku ya kufa kwake. 8 Ndipo huyo Manoa akamwomba Bwana, akisema, Ee Bwana, nakuomba, yule mtu wa Mungu uliyemtuma na aje kwetu mara ya pili, atufundishe hayo yatupasayo kumfanyia huyo mtoto atakayezaliwa. 9 Mungu akasikiza sauti ya Manoa; naye malaika wa Mungu akamwendea yule mwanamke tena alipokuwa anaketi shambani; lakini mumewe, Manoa, hakuwapo pamoja naye. 10 Basi huyo mwanamke akaenda haraka, akapiga mbio, na kumwambia mumewe, akisema, Tazama, huyo mtu amenitokea, huyo aliyenijilia siku ile. 11 Basi Manoa akainuka, akamwandama mkewe, na kumfikilia mtu huyo, akamwuliza, Je! Wewe ndiwe mtu yule aliyenena na huyu mwanamke? Akasema, Naam, ni mimi. 12 Manoa akasema, Basi sasa hayo maneno yako yatakapotimia, je! Huyo mtoto atakuwa wa namna gani, na kazi yake itakuwa ni nini? 13 Malaika wa Mungu akamwambia Manoa, Katika hayo yote niliyomwambia huyo mwanamke na ajihadhari. 14 Asile kitu cho chote kitokacho katika mzabibu, wala asinywe divai, wala mvinyo, wala asile kitu cho chote kilicho najisi; hayo yote niliyomwamuru na ayatunze. 15 Kisha Manoa akamwambia huyo malaika wa Bwana, Nakuomba, tukuzuie, ili tupate kuandaa mwana-mbuzi kwa ajili yako. 16 Lakini malaika wa Bwana akamwambia Manoa, Ujapokuwa wanizuia, sitakula katika mkate wako; na kwamba wataka kufanya tayari sadaka ya kuteketezwa, inakupasa kumsongezea Bwana. Kwa kuwa Manoa hakujua ya kwamba yeye ni malaika wa Bwana. 17 Manoa akamwambia huyo malaika wa Bwana, Jina lako ni nani, ili kwamba hapo hayo maneno yako yatakapotimia nipate kukutukuza? 18 Huyo malaika wa Bwana akamwambia, Kwani wewe kuniuliza jina langu, kwa kuwa jina hilo ni la ajabu? 19 Basi Manoa akamtwaa yule mwana-mbuzi, pamoja na sadaka ya unga, akamtolea Bwana hapo juu ya mwamba; huyo malaika akatenda la ajabu; Manoa na mkewe wakaangalia. 20 Kwa maana, ikawa, mara huo mwali wa moto ulipopaa juu mbinguni kutoka pale madhabahuni, huyo malaika wa Bwana akapaa katika mwali wa moto wa madhabahu; nao Manoa na mkewe wakaangalia; wakainama kifudifudi. 21 Lakini malaika wa Bwana hakumtokea Manoa tena, wala mkewe. Ndipo Manoa alipojua ya kwamba ndiye malaika wa Bwana. 22 Manoa akamwambia mkewe, Hakika yetu tutakufa sisi, kwa sababu tumemwona Mungu. 23 Lakini mkewe akamwambia, Kama Bwana angetaka kutuua hangepokea sadaka ya kuteketezwa, wala sadaka ya unga, mikononi mwetu, wala hangetuonyesha mambo hayo yote, wala hangetuambia mambo kama hayo wakati huu. 24 Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. 25 Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.

Waamuzi 14

1 Samsoni akatelemkia Timna, akaona mwanamke huko Timna, mmojawapo wa binti za Wafilisti. 2 Kisha akapanda, akawaambia baba yake na mama yake, akasema, Nimemwona mwanamke huko Timna, mmojawapo wa binti za Wafilisti; basi mnipatie, nimwoe. 3 Ndipo baba yake na mama yake wakamwambia, Je! Hapana mwanamke hata mmoja katika ndugu zako, au katika jamaa zangu zote, hata uende kumwoa mwanamke kwa hawa Wafilisti wasiotahiriwa? Samsoni akamwambia baba yake; Mnipatie huyo, kwa maana ananipendeza sana. 4 Lakini baba yake na mama yake hawakujua ya kuwa jambo hili ni la Bwana; maana alitaka kisa juu ya Wafilisti. Basi wakati ule Wafilisti walikuwa wakiwatawala Israeli. 5 Ndipo Samsoni na baba yake na mama yake wakatelemkia Timna, wakafika mashamba ya mizabibu huko Timna; na tazama, mwana-simba akamngurumia. 6 Roho ya Bwana ikamjilia kwa nguvu, naye akampasua kana kwamba anampasua mwana-mbuzi, wala hakuwa na kitu cho chote mkononi mwake; lakini hakuwaambia baba yake na mama yake aliyoyafanya. 7 Basi akatelemka na kuzungumza na huyo mwanamke; naye akampendeza Samsoni sana. 8 Kisha baadaye akarudi ili kumtwaa, naye akageuka kando kuuangalia mzoga wa huyo simba; na tazama, nyuki wengi walikuwamo ndani ya mzoga wa simba, na asali. 9 Akatwaa asali mikononi mwake akaenda mbele, huku akila alipokuwa akienenda, akawafikilia babaye na mamaye, akawapa, nao wakala; lakini hakuwaambia ya kuwa ameitwaa hiyo asali katika mzoga wa simba. 10 Basi babaye akamtelemkia huyo mwanamke; Samsoni naye akafanya karamu huko; kwa kuwa vijana ndivyo walivyokuwa wakifanya. 11 Basi ikawa hapo walipomwona, wakamletea wenziwe thelathini, wawe pamoja naye. 12 Samsoni akawaambia, Mimi nitawategea ninyi kitendawili; kama mwaweza kunionyesha katika hizo siku saba za karamu, na kukitambua, ndipo hapo nitawapa mavazi thelathini ya kitani na mavao mengine thelathini; 13 lakini msipoweza kunionyesha ndipo hapo ninyi mtanipa mimi mavazi thelathini ya kitani na mavao mengine thelathini. Basi wakamwambia, Haya, tega kitendawili chako, ili tupate kukisikia. 14 Naye akawaambia, Katika huyo mwenye kula kikatoka chakula, Katika huyo mwenye nguvu ukatoka utamu. 15 Ikawa kwa siku ya saba, wakamwambia mkewe Samsoni, Mbembeleze mumeo, ili atuonyeshe hicho kitendawili, tusije tukakuteketeza moto wewe na nyumba ya baba yako; je! Mmetuita ili mpate kuichukua mali yetu? Je! Sivyo? 16 Basi mkewe Samsoni akalia mbele yake, akasema, Wewe wanichukia tu, wala hunipendi; wewe umewategea kitendawili hao wana wa watu wangu, nawe hukuniambia mimi. Naye akamwambia, Angalia, sikumwambia baba yangu wala mama yangu, nami nikuambie wewe? 17 Naye akalia mbele yake hizo siku saba, wakati ulioendelea karamu yao; basi ikawa siku ya saba akamwambia, kwa sababu alikuwa akimsisitiza sana; naye akawaambia wale wana wa watu wake hicho kitendawili. 18 Nao watu wa mji wakamwambia siku ya saba kabla ya jua kuchwa,Ni kitu gani kilicho tamu kuliko asali? Ni kitu gani kilicho na nguvu kuliko simba? Naye akawaambia, kwamba hamkulima na mtamba wangu,Hamngekitambua kitendawili changu. 19 Roho ya Bwana ikamjilia juu yake kwa nguvu, naye akatelemkia Ashkeloni, akapiga watu waume thelathini katika watu hao, na kuzitwaa nyara zao, na kuwapa hao waliokitambua kitendawili mavao hayo. Hasira zake zikamwaka, naye akakwea kwenda nyumbani kwa baba yake. 20 Lakini huyo mke wa Samsoni aliozwa mwenzake, ambaye alikuwa amemtendea kama rafikiye.

Waamuzi 15

1 Lakini ikawa baadaye, wakati wa mavuno ya ngano Samsoni akaenda kumtazama mkewe, akamchukulia mwana-mbuzi; akasema, Nitaingia chumbani kwa mke wangu. Lakini baba yake mwanamke hakumwacha kuingia. 2 Baba yake akasema, Hakika mimi nalidhani ya kuwa umemchukia kabisa; basi nalimpa rafiki yako. Je! Ndugu yake mdogo mzuri kuliko yeye? Tafadhali, mtwae huyo badala yake. 3 Samsoni akasema, Safari hii nitakuwa sina hatia katika habari za hawa Wafilisti, hapo nitakapowadhuru. 4 Samsoni akaenda akakamata mbweha mia tatu; kisha akatwaa vienge vya moto akawafunga mbweha mkia kwa mkia, akatia kienge kati ya kila mikia miwili. 5 Alipokwisha kuviwasha moto vile vienge, akawaachia mbweha kati ya ngano ya Wafilisti, akayateketeza matita, na ngano, hata na mashamba ya mizeituni. 6 Ndipo Wafilisti wakasema, Ni nani aliyetenda hivi? Wakasema, Ni huyo Samsoni, mkwewe yule Mtimna, kwa sababu alimchukua mkewe akampa mwenzake. Wafilisti wakaenda wakamteketeza yeye na baba yake kwa moto. 7 Samsoni akawaambia, Ikiwa ninyi mnafanya mambo kama hayo, hakika nitajilipiza kisasi juu yenu, na baadaye nitakoma. 8 Akawapiga upeo, mapigo makuu sana, kisha akatelemka akakaa katika ufa wa jabali la Etamu. 9 Basi Wafilisti wakapanda wakapiga kambi yao katika Yuda, wakajieneza katika Lehi. 10 Watu wa Yuda wakasema, Mbona mmekuja kupigana nasi? Wakasema, Tumepanda ili kumfunga Samsoni, kumtenda yeye kama alivyotutenda sisi. 11 Ndipo watu elfu tatu wa Yuda wakatelemka hata ule ufa wa jabali la Etamu, wakamwambia Samsoni, Je! Hujui ya kuwa Wafilisti wanatutawala? Ni nini hii, basi, uliyotutenda? Akawaambia, Kadiri ile walivyonitenda mimi, ndivyo nilivyowatenda wao. 12 Wakamwambia, Tumeshuka ili kukufunga, tupate kukutia katika mikono ya Wafilisti. Samsoni akawaambia, Niapieni ya kwamba ninyi wenyewe hamtaniangukia. 13 Wakamwambia, wakisema, Vema, lakini tutakufunga sana, na kukutia katika mikono yao; lakini hakika hatutakuua. Basi wakamfunga kwa kamba mbili mpya, wakamchukua kutoka huko jabalini. 14 Alipofika Lehi, Wafilisti wakapiga kelele walipokutana naye; ndipo roho ya Bwana ikamjia kwa nguvu, na zile kamba zilizokuwa juu ya mikono yake zikawa kama kitani iliyoteketezwa kwa moto, na vile vifungo vyake vikaanguka mikononi mwake. 15 Naye akaona mfupa mbichi wa taya ya punda, akautwaa, akapiga watu elfu kwa mfupa huo; 16 Samsoni akasema, Kwa taya ya punda chungu juu ya chungu, Kwa taya ya punda nimepiga watu elfu. 17 Ikawa, alipokuwa amekwisha kunena akautupa ule mfupa wa taya mkononi mwake; na mahali pale pakaitwa Ramath-lehi. 18 Kisha akaona kiu sana, akamwita Bwana akasema, Wewe umetupa wokovu huu kwa mkono wa mtumishi wako; na sasa nitakufa kwa kiu, na kuanguka katika mikono ya watu wasiotahiriwa. 19 Lakini Mungu akapasua mahali penye shimo palipo katika Lehi, pakatoka maji; naye alipokwisha kunywa, roho yake ikamrudia, akaburudika; kwa hiyo jina la mahali pale likaitwa Enhakore, napo pa katika Lehi hata hivi leo. 20 Naye akawa mwamuzi wa Israeli: katika siku za Wafilisti muda wa miaka ishirini.

Waamuzi 16

1 Samsoni akaenda Gaza, akaona huko mwanamke kahaba, akaingia kwake. 2 Watu wa Gaza wakaambiwa, ya kwamba, huyo Samsoni amekuja huku. Wakamzingira, wakamvizia usiku kucha, penye lango la mji, wakanyamaza kimya usiku kucha, wakisema, Na tungoje mpaka mapambazuko, ndipo tutamwua. 3 Basi Samsoni akalala hata usiku wa manane, akaondoka katikati ya usiku, akaishika milango ya lango la mji, na miimo yake miwili, akaing'oa pamoja na komeo lake, akajitwika mabegani, akavichukua hata kilele cha mlima ule unaokabili Hebroni. 4 Ikawa baada ya hayo akampenda mwanamke mmoja katika bonde la Soreki, jina lake akiitwa Delila. 5 Nao wakuu wa Wafilisti wakamwendea, wakamwambia, Mbembeleze, upate kujua asili ya nguvu zake nyingi, na jinsi tutakavyoweza kumshinda, tupate kumfunga na kumtesa; nasi tutakupa kila mtu fedha elfu na mia moja. 6 Delila akamwambia Samsoni, Tafadhali uniambie asili ya nguvu zako nyingi, na jinsi uwezavyo kufungwa, ili uteswe. 7 Samsoni akamwambia, Wakinifunga kwa kamba mbichi saba ambazo hazijakauka bado, hapo ndipo nitakuwa dhaifu, nitakuwa kama wanadamu wenzangu. 8 Ndipo wakuu wa Wafilisti wakamletea kamba mbichi saba zisizokauka, naye akamfunga nazo. 9 Na yule mwanamke alikuwa na watu katika chumba cha ndani, wakimwotea. Basi akamwambia Samsoni, Wafilisti wanakujia. Ndipo akazikata zile kamba kama vile uzi wa pamba ukatwavyo ukiguswa na moto. Basi hiyo asili ya nguvu zake haikujulikana. 10 Delila akamwambia Samsoni, Tazama, umenidhihaki, na kuniambia uongo; sasa tafadhali, niambie, waweza kufungwa kwa kitu gani? 11 Akamwambia Wakinifunga tu kwa kamba mpya ambazo mtu hakufanya kazi nazo, hapo ndipo nitakuwa dhaifu, nitakuwa kama wanadamu wenzangu. 12 Basi Delila akatwaa kamba mpya akamfunga nazo, akamwambia, Wafilisti wanakujia, Samsoni. Na wale wenye kuotea walikuwa katika chumba cha ndani. Naye akazikata, akazitupa kutoka mikononi mwake kama uzi. 13 Delila akamwambia Samsoni, Hata sasa umenidhihaki, umeniambia maneno ya uongo; niambie sasa, waweza kufungwa kwa kitu gani? Akamwambia, Ukivifuma hivi vishungi saba vya nywele za kichwa changu katika mtande wa nguo. 14 Basi akazifunga kwa msumari, akamwambia Samsoni, Wafilisti wanakujia. Naye akaamka usingizini, akaung'oa ule msumari, na ule mtande. 15 Mwanamke akamwambia, Wawezaje kusema, Nakupenda; na moyo wako haupo pamoja nami? Umenidhihaki mara hizi tatu, wala hukuniambia asili ya nguvu zako nyingi. 16 Ikawa, kwa vile alivyomsumbua kwa maneno yake kila siku, na kumwudhi, roho yake ikadhikika hata kufa. 17 Ndipo alipomwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akamwambia, Wembe haukupita juu ya kichwa changu kamwe; maana mimi nimekuwa Mnadhiri wa Mungu, tangu tumboni mwa mama yangu; nikinyolewa, ndipo nguvu zangu zitanitoka, nami nitakuwa dhaifu, nitakuwa kama wanadamu wenzangu. 18 Delila alipoona ya kuwa amemwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akatuma mtu akawaita wakuu wa Wafilisti, akisema, Njoni huku mara hii tu, maana ameniambia yote aliyo nayo moyoni mwake. Ndipo wakuu wa Wafilisti wakamwendea wakachukua ile fedha mikononi mwao. 19 Naye akamlaza usingizi magotini pake. Kisha akamwita mtu akavinyoa vile vishungi saba vya nywele za kichwa chake; akaanza kumsumbua, nguvu zake zikamtoka. 20 Kisha akasema, Samsoni, Wafilisti wanakujia. Akaamka katika usingizi wake, akasema, Nitakwenda nje kama siku nyingine, na kujinyosha. Lakini hakujua ya kuwa Bwana amemwacha. 21 Wafilisti wakamkamata, wakamng'oa macho; wakatelemka naye mpaka Gaza, wakamfunga kwa vifungo vya shaba; naye alikuwa akisaga ngano katika gereza. 22 Lakini zile nywele za kichwa chake zikaanza kukua tena baada ya kunyolewa kwake. 23 Kisha wakuu wa Wafilisti wakakusanyika ili kumtolea sadaka Dagoni mungu wao, na kufurahi; maana walisema, Mungu wetu amemtia Samsoni adui wetu mikononi mwetu. 24 Na hao watu walipomwona wakamhimidi mungu wao, maana walisema, Mungu wetu amemtia mikononi mwetu huyu adui wetu, aliyeiharibu nchi yetu na kuwaua watu wengi miongoni mwetu. 25 Ikawa mioyo yao iliposhangilia, wakasema, Mwiteni Samsoni, ili atufanyie michezo. Basi wakamwita Samsoni atoke gerezani, akacheze mbele yao wakamweka katikati ya nguzo mbili. 26 Samsoni akamwambia yule kijana aliyemshika mkono, Niache nizipapase nguzo ambazo nyumba hii inazikalia, nipate kuzitegemea. 27 Basi nyumba ile ilikuwa imejaa watu waume kwa wake; na wakuu wote wa Wafilisti walikuwamo humo, na juu ya dari palikuwa na watu elfu tatu waume kwa wake waliokuwa wakitazama, wakati Samsoni alipocheza. 28 Samsoni akamwita Bwana, akasema, Ee Bwana MUNGU, unikumbuke, nakuomba, ukanitie nguvu, nakuomba, mara hii tu, Ee Mungu, ili nipate kujilipiza kisasi juu ya Wafilisti kwa ajili ya macho yangu mawili. 29 Kisha Samsoni akazishika nguzo mbili za katikati ambazo nyumba ile ilikaa juu yake, akazitegemea, moja kwa mkono wake wa kuume na moja kwa mkono wake wa kushoto. 30 Samsoni akasema; Na nife pamoja na hawa Wafilisti. Akainama kwa nguvu zake zote; ile nyumba ikawaangukia hao wakuu, na watu wote waliokuwa ndani yake. Basi wale watu aliowaua wakati wa kufa kwake walikuwa wengi kuliko wale aliowaua wakati wa uhai wake. 31 Ndipo ndugu zake, na watu wote wa nyumba ya baba yake wakatelemka, wakamtwaa wakamchukua, wakamzika kati ya Sora na Eshtaoli, katika kiwanja cha kuzikia cha Manoa baba yake. Naye alikuwa mwamuzi wa Israeli muda wa miaka ishirini.

Waamuzi 17

1 Wakati huo alikuwako mtu mmoja wa nchi ya vilima ya Efraimu, ambaye jina lake alikuwa akiitwa Mika. 2 Naye akamwambia mama yake, Hizo fedha elfu na mia moja ulizonyang'anywa, ambazo uliweka kiapo kwa ajili yake na kusema masikioni mwangu, tazama, ninazo mimi hizo fedha; ni mimi niliyezitwaa. Mama yake akasema, mwanangu na abarikiwe na Bwana. 3 Basi akamrudishia mama yake hizo fedha elfu na mia moja. Mama yake akasema, Mimi naziweka fedha hizi kabisa ziwe wakfu kwa Bwana, zitoke mkononi mwangu kwa ajili ya mwanangu, ili kufanya sanamu ya kuchonga, na sanamu ya kusubu; basi kwa hiyo nakurudishia wewe. 4 Basi hapo alipomrudishia mama yake hizo fedha, mama yake akatwaa fedha mia mbili, akampa fundi mwenye kusubu fedha, naye akafanya sanamu ya kuchonga kwazo, na sanamu ya kusubu; ambazo zilikuwa ndani ya nyumba ya Mika. 5 Basi mtu huyo Mika alikuwa na nyumba ya miungu, naye akafanya naivera, na kinyago, akamweka wakfu mmoja miongoni mwa wanawe, akawa kuhani wake. 6 Siku hizo hapakuwa na mfalme katika israeli; kila mtu alifanya hayo aliyoyaona kuwa ni mema machoni pake mwenyewe. 7 Alikuwako mtu mmoja hirimu aliyetoka Bethlehemu-yuda, wa jamaa ya Yuda, aliyekuwa ni Mlawi, naye akakaa huko hali ya ugeni. 8 Mtu huyo akatoka katika huo mji, katika Bethlehemu-yuda, ili aende kukaa hali ya ugeni hapo atakapoona mahali; akafikilia nchi ya vilima vilima ya Efraimu katika safari yake, hata nyumba ya huyo Mika. 9 Mika akamwuliza, Watoka wapi wewe? Akamwambia, Mimi ni Mlawi wa Bethlehemu-yuda, nami naenda kukaa hali ya ugeni po pote nitakapoona mahali. 10 Mika akamwambia, kaa pamoja nami, uwe kwangu baba, tena kuhani, nami nitakupa fedha kumi mwaka kwa mwaka, na nguo ya kuvaa, na vyakula. Basi huyo Mlawi akaingia ndani. 11 Huyo Mlawi aliridhika kukaa na mtu huyo; kisha huyo hirimu akawa kwake kama wanawe mmojawapo. 12 Basi Mika akamweka wakfu huyo Mlawi, huyo hirimu, naye akawa kuhani wake, akakaa nyumbani mwa Mika. 13 Ndipo Mika akasema, Sasa najua ya kwamba Bwana atanitendea mema, kwa kuwa nina Mlawi kuwa kuhani wangu.

Waamuzi 18

1 Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; tena katika siku hizo kabila ya Wadani wakajitafutia urithi wapate mahali pa kukaa; maana hata siku hiyo urithi wao haujawaangukia kati ya kabila za Israeli. 2 Basi wana wa Dani wakatuma watu wa jamaa zao, watu watano katika hesabu yao yote, watu mashujaa, kutoka Sora, na kutoka Eshtaoli, ili kuipeleleza hiyo nchi, kuiaua; wakawaambia, Haya, endeni mkaikague nchi hii; basi wakaifikilia nchi ya vilima vilima ya Efraimu, hata nyumba ya huyo Mika, Wakalala huko. 3 Basi hapo walipokuwa karibu na nyumba ya Mika, wakatambua sauti yake huyo hirimu, huyo Mlawi; ndipo wakageuka wakaenda kuko, na kumwuliza, Je! Ni nani aliyekuleta wewe huku? Nawe wafanya nini mahali hapa? Una kazi gani hapa? 4 Naye akawaambia, Hivi na hivi ndivyo alivyonifanyia Mika, ameniajiri, nami nimekuwa kuhani wake. 5 Nao wakamwambia, Tafadhali tutakie shauri la Mungu, ili tupate kujua kwamba njia yetu tuiendeayo itafanikiwa. 6 Kuhani akawaambia, Haya endeni na amani; njia mnayoiendea i mbele za Bwana. 7 Ndipo hao watu watano wakaenda zao, wakafika Laisha, wakawaona wale watu waliokuwamo ndani yake, jinsi walivyokaa salama salimini kwa mfano wa walivyokaa hao Wasidoni, wenye starehe na hifadhi, kwa maana hapakuwa na mtu katika nchi hiyo aliyekuwa na amri, aliyeweza kuwatweza katika neno lo lote, nao walikuwa wa mbali na hao Wasidoni, wala hawakuwa na shughuli na mtu ye yote. 8 Kisha wakawarudia ndugu zao huko Sora na Eshtaoli; ndugu zao wakawauliza; Haya, mna habari gani? 9 Wakasema, Haya, inukeni, twende tukapigane nao; kwa maana tumeiona hiyo nchi nayo ni nchi nzuri sana; nanyi, je! Mwanyamaa tu? Msiwe wavivu kwenda, na kuingia, ili mpate kuimiliki nchi hiyo. 10 Hapo mtakapokwenda mtawafikilia watu wakaao salama salimini, na hiyo nchi nayo ni kubwa; kwa kuwa Mungu ameitia mikononi mwenu; ni mahali ambapo hapana kupungukiwa na kitu cho chote kilicho duniani. 11 Basi wakatoka hapo watu mia sita waliovaa silaha za vita, wa jamaa ya Wadani, kutoka Sora, na kutoka Eshtaoli. 12 Wakakwea juu na kupiga kambi huko Kiriath-yearimu, katika Yuda; kwa sababu hiyo wakapaita mahali pale jina lake Mahane-dani hata hivi leo; tazama, ni hapo nyuma ya Kiriath-yearimu. 13 Nao wakapita huko hata hiyo nchi ya vilima vilima ya Efraimu, wakafikilia nyumba ya huyo Mika. 14 Ndipo hao watu watano waliokwenda kuipeleleza nchi ya Laisha wakajibu, na kuwaambia ndugu zao Je! Ninyi mwajua ya kwamba mna naivera ndani ya nyumba hizi, na kinyago na sanamu ya kuchonga, na sanamu ya kusubu? Basi sasa fikirini iwapasayo kufanya. 15 Basi wakageuka wakaenda kuko, wakafikilia nyumba ya huyo hirimu, Mlawi, hata hiyo nyumba ya Mika, nao wakamwuliza habari za hali yake. 16 Hao watu mia sita wenye kuvaa silaha zao za vita, waliokuwa ni wana wa Dani, wakasimama penye maingilio ya lango. 17 Na hao watu watano waliokwenda kuipeleleza hiyo nchi wakakwea juu, wakaingia ndani, na kuitwaa hiyo sanamu ya kuchonga, na hiyo naivera, na kile kinyago, na hiyo sanamu ya kusubu; na huyo kuhani akasimama penye maingilio ya lango pamoja na hao watu waume sita mia wenye kuvaa silaha za vita. 18 Nao hapo walipoingia ndani ya nyumba ya Mika, na kuileta hiyo sanamu ya kuchonga, na hiyo naivera, na kile kinyago, na hiyo sanamu ya kusubu, huyo kuhani akawauliza, Je! Mwafanya nini ninyi? 19 Wao wakamwambia, Nyamaza wewe, weka mkono wako kinywani mwako, uende pamoja nasi, uwe kwetu baba, tena kuhani; je! Ni vema kwako kuwa kuhani kwa ajili ya nyumba ya mtu mmoja, au kuwa kuhani kwa ajili ya kabila na jamaa katika Israeli? 20 Huyo kuhani moyo wake ukafurahi, naye akaitwaa hiyo naivera, na kile kinyago, na hiyo sanamu ya kuchonga, akaenda katikati ya hao watu. 21 Basi wakageuka wakaenda zao, lakini watoto wadogo na wanyama wao wa mifugo, na vyombo vyao, wakawatanguliza mbele yao. 22 Walipokuwa wamekwenda kitambo kizima kutoka nyumba ya Mika, wale watu waliokuwa katika nyumba zilizokuwa karibu na nyumba ya Mika walikutana, wakawaandama na kuwapata hao wana wa Dani. 23 Wakawapigia kelele wana wa Dani. Nao wakageuza nyuso zao na kumwambia Mika, Una nini wewe, hata ukaja na mkutano namna hii? 24 Akasema, Ninyi mmeichukua miungu niliyoifanya, na huyo kuhani, nanyi mmekwenda zenu, nami nina nini tena? Basi imekuwaje ninyi kuniuliza, Una nini wewe? 25 Hao wana wa Dani wakamwambia, Hiyo sauti yako isisikiwe kati yetu, wasije walio na hasira wakakuangukia, nawe ukapotewa na uhai wako, pamoja na uhai wa watu wa nyumbani mwako. 26 Basi wana wa Dani wakaenda zao; naye Mika alipoona ya kuwa ni wenye nguvu kumshinda yeye, akageuka akarudi nyumbani kwake. 27 Nao wakakitwaa hicho alichokuwa amekifanya Mika, na kuhani aliyekuwa naye nao wakafikilia Laisha, kwenye watu waliokuwa wenye starehe na hifadhi, wakawapiga kwa makali ya upanga; wakaupiga moto mji wao. 28 Wala hakuwako mwokozi, kwa sababu huo mji ulikuwa ni mbali sana na Sidoni, nao hawakuwa na shughuli na mtu awaye yote; na mji huo ulikuwa katika hilo bonde lililo karibu na Bethrehobu. Nao wakaujenga huo mji na kukaa humo. 29 Wakauita mji jina lake Dani, kwa kuliandama jina la baba yao Dani, aliyezaliwa kwake Israeli; lakini jina la mji huo hapo kwanza ulikuwa ukiitwa Laisha. 30 Kisha wana wa Dani wakajisimamishia hiyo sanamu ya kuchonga; na Yonathani mwana wa Gershomu, mwana wa Musa, yeye na wanawe walikuwa ni makuhani katika kabila ya Wadani hata siku ya kuchukuliwa mateka hiyo nchi. 31 Basi wakajisimamishia hiyo sanamu ya kuchonga aliyoifanya Mika, wakati wote ile nyumba ya Mungu ilipokuwako huko Shilo.

Waamuzi 19

1 Ikawa katika siku hizo, hapo kulipokuwa hapana mfalme katika Israeli, alikuwapo Mlawi mmoja aliyekuwa akikaa hali ya ugeni upande wa mbele wa nchi ya vilima vilima ya Efraimu, aliyejitwalia suria katika Bethlehemu-yuda. 2 Kisha huyo suria yake akaandama ukahaba kinyume chake, kumwacha kwenda nyumbani kwa baba yake huko Bethlehemu-yuda, akakaa kuko muda wa miezi minne. 3 Kisha mumewe akainuka akamfuata, aseme naye kwa upendo, ili apate kumrudisha tena, naye alikuwa na mtumishi wake pamoja naye na punda wawili; huyo mwanamke akamkaribisha katika nyumba ya baba yake; naye baba yake alipomwona akafurahi kuonana naye. 4 Kisha mkwewe, babaye huyo mwanamke, akamzuia; akakaa naye siku tatu; basi wakala na kunywa na kulala kuko. 5 Kisha ilikuwa siku ya nne, wakaamka asubuhi na mapema, naye akaondoka ili aende zake; baba yake huyo mwanamke akamwambia mkwewe, Tuza moyo wako, ule chakula kidogo, kisha baadaye mtakwenda zenu. 6 Basi wakaketi, wakala na kunywa wote wawili pamoja; kisha baba yake mwanamke akamwambia huyo mtu, Uwe radhi, tafadhali, ukae usiku kucha, na moyo wako na ufurahi. 7 Yule mtu akainuka ili aondoke; lakini mkwewe akamsihi-sihi, naye akalala kuko tena. 8 Basi akaamka asubuhi na mapema siku ya tano ili aende zake; na baba yake mwanamke akasema, Tuza moyo wako, tafadhali, ukae hata jua lipinduke; nao wakala chakula wote wawili. 9 Kisha hapo mtu huyo alipoinuka ili aende zake, yeye na suria yake, na mtumishi wake, huyo mkwewe, baba yake mwanamke, akamwambia, Tazama mchana wakaribia jioni, tafadhali kaa usiku kucha; tazama mchana wakaribia mwisho wake, lala hapa, ili moyo wako ufurahi; hata kesho uende zako asubuhi na mapema, ili upate kwenda kwenu. 10 Lakini huyo mtu hakukubali kukaa usiku huo, ila akainuka, akaenda zake, akafika mkabala wa Yebusi (huo ndio Yerusalemu); nao walikuwako pamoja naye punda wawili waliotandikwa; suria yake naye alikuwa pamoja naye. 11 Basi hapo walipokuwa karibu na Yebusi, mchana ulikuwa umeendelea mno; yule mtumishi akamwambia bwana wake, Haya, tafadhali, tugeuke kando na kuingia mji huu wa Wayebusi, tulale humu. 12 Bwana wake akamwambia, Hatutageuka sisi kuingia mji wa wageni, ambao si wa wana wa Israeli; lakini tutapita mpaka Gibea. 13 Kisha akamwambia mtumishi wake, Haya, tuifikilie miji hii mmojawapo nasi tutalala katika Gibea au katika Rama. 14 Basi wakashika njia kwenda zao mbele; jua likawachwea walipokuwa karibu na Gibea, ambao ni mji wa Benyamini. 15 Wakageuka huko, wapate kuingia na kulala katika Gibea; akaingia ndani, akaketi katika njia kuu ya mji; kwa kuwa hapakuwa na mtu awaye yote aliyewakaribisha nyumbani kwake kulala. 16 Kisha, tazama, akatokea mtu mume mzee, atoka kazini kwake shambani, wakati wa jioni; mtu huyo alikuwa ni wa ile nchi ya vilima vilima ya Efraimu, naye alikuwa anakaa katika Gibea hali ya ugeni lakini wenyeji wa mahali hapo walikuwa Wabenyamini. 17 Naye alipovua macho yake, akamwona huyo mtu msafiri katika njia kuu ya mji; huyo mzee akamwuliza, Waenda wapi wewe? Nawe watoka wapi? 18 Akamwambia, Sisi twapita hapa kutoka Bethlehemu-yuda, twaenda huko upande wa mbali wa nchi ya vilima vilima ya Efraimu; ndiko nilikotoka nami nilikwenda Bethlehemu-yuda; nami sasa naiendea nyumba ya Bwana wala hapana mtu anikaribishaye nyumbani mwake. 19 Walakini nyasi tunazo, na chakula cha hawa punda zetu; mkate pia tunao na divai kwa mimi na huyu kijakazi wako, na kwa huyu kijana aliye pamoja nasi watumishi wako; hapana uhitaji wa kitu cho chote. 20 Kisha huyo mzee alisema, Na iwe amani kwako; lakini na haya yaliyokupungukia na yawe juu yangu mimi lakini usilale njiani. 21 Basi akamtia ndani ya nyumba yake, akawapa punda chakula; nao wakaosha miguu, wakala na kunywa. 22 Hapo walipokuwa wakifurahisha mioyo yao, tazama, watu wa mji huo, watu mabaradhuli wakaizingira hiyo nyumba pande zote, wakagonga mlango; wakasema na huyo mwenye nyumba, huyo mzee, na kumwambia, Mlete nje mtu yule aliyefika nyumbani kwako, ili tupate kumjua. 23 Naye mtu mwenye nyumba akawatokea hapo nje, na kuwaambia, La, sivyo, ndugu zangu nawasihi msifanye uovu jinsi hii; kwa kuwa mtu huyu ameingia ndani ya nyumba yangu, msifanye upumbavu huu. 24 Tazama, binti yangu yupo hapa, ni mwanamwali, na suria wake huyo mtu; nitawaleta hapa nje sasa nanyi watwezeni, na kuwatenda hayo myaonayo kuwa ni mema; lakini mtu huyu msimtende jambo la upumbavu namna hii. 25 Lakini hao watu hawakukubali kumsikia; basi mtu huyo akamshika suria wake, na kumleta nje kwao; nao wakamjua, na kumtenda uovu usiku kucha hata asubuhi kisha kulipoanza kupambauka wakamwacha aende zake. 26 Ndipo huyo mwanamke akaja alfajiri, akaanguka chini mlangoni pa nyumba ya mtu yule alimokuwamo bwana wake, hata kulipokucha. 27 Bwana wake akaondoka asubuhi, akaifungua milango ya nyumba, akatoka nje ili aende zake, na tazama, huyo mwanamke suria yake alikuwa ameanguka pale mlangoni pa nyumba, na mikono yake ilikuwa i pale kizingitini. 28 Akamwambia, Haya ondoka, twende zetu; lakini hakuna aliyemjibu; ndipo akamwinua akamweka juu ya punda; mtu huyo akaondoka, akaenda mahali pake mwenyewe. 29 Naye alipokwisha kuingia nyumbani mwake, akatwaa kisu, kisha akamshika huyo suria yake, akampasua kiungo kwa kiungo, vipande kumi na viwili akampeleka katika mipaka yote ya Israeli. 30 Basi ikawa, wote walioliona jambo hilo wakasema, Jambo kama hili halijatendeka wala kuonekana tangu siku hiyo wana wa Israeli walipokwea kutoka katika nchi ya Misri hata leo; haya, lifikirini, fanyeni shauri, mkanene.

Waamuzi 20

1 Ndipo wana wa Israeli walipotoka; na mkutano ukakutanika kama mtu mmoja, kutoka Dani hata Beer-sheba, pamoja na nchi ya Gileadi wakamkutanikia Bwana huko Mispa. 2 Hao wakuu wa watu, maana wakuu wa kabila zote za Israeli, wakajihudhurisha katika huo mkutano wa watu wa Mungu, watu waume mia nne elfu waendao kwa miguu, wenye kutumia upanga. 3 Basi wana wa Benyamini walipata habari ya kuwa wana wa Israeli wamekwea kwenda Mispa. Wana wa Israeli wakasema, Tuambieni huo uovu ulikuwaje kutendeka? 4 Huyo Mlawi, huyo mume wa mwanamke aliyeuawa, akajibu na kusema, Mimi nilifikilia Gibea ulio wa Benyamini mimi na suria yangu, ili tulale. 5 Nao watu waume wa Gibea wakaniondokea, na kuizingira hiyo nyumba pande zote juu yangu wakati wa usiku; walidhani kuniua, na suria wangu wakamtenza nguvu, hata amekufa. 6 Basi nikamtwaa huyo suria yangu, na kumkata vipande, na kumpeleka katika nchi yote ya urithi wa Israeli; kwa sababu wametenda maovu makuu na upumbavu katika Israeli. 7 Angalieni, ninyi wana wa Israeli nyote, sasa toeni maneno na mashauri yenu. 8 Basi watu hao wote waliinuka kama mtu mmoja, wakisema, Hatutakwenda, hata mmoja, hemani kwake, wala hatutaondoka, hata mmoja, kwenda nyumbani kwake. 9 Lakini jambo tutakalowatenda watu wa Gibea ni hili; tutakwea kwa kura kwenda kuupiga; 10 nasi tutatwaa watu kumi katika mia katika kabila zote za Israeli, na watu mia katika elfu, na watu elfu katika elfu kumi, ili waende kuwatwalia watu vyakula, ili kwamba, hapo watakapofika Gibea ya Benyamini wapate kutenda mfano wa upumbavu huo wote walioutenda wao katika Israeli. 11 Basi waume wote wa Israeli walikutana pamoja juu ya mji huo, walikuwa wanashikamana pamoja kama mtu mmoja. 12 Kisha kabila za Israeli wakatuma watu waende katika kabila yote ya Benyamini, wakasema, Je! Ni uovu gani huu uliokuwa kati yenu? 13 Basi sasa watoeni watu hao, hao mabaradhuli walio katika Gibea, ili kwamba tupate kuwaua, na kuuondoa uovu katika Israeli. Lakini Benyamini hawakukubali kuisikia sauti ya ndugu zao wana wa Israeli. 14 Lakini wana wa Benyamini wakakutanika huko Gibea kutoka katika miji yao, ili watoke kwenda kupiga vita juu ya wana wa Israeli. 15 Hao wana wa Benyamini walihesabiwa siku ile kutoka hiyo miji, watu waume ishirini na sita elfu waliotumia upanga, zaidi ya hao waliokaa Gibea, ambao walihesabiwa watu wateule mia saba. 16 Katika watu hao wote walikuwako watu waume mia saba waliochaguliwa, wenye shoto; kila mmoja alikuwa anaweza kuutupia unywele mawe kwa teo, wala asikose. 17 Nao watu wa Israeli, mbali na hao wa Benyamini, walihesabiwa kuwa ni watu waume mia nne elfu, wenye kutumia upanga; hao wote walikuwa ni watu wa vita. 18 Basi wana wa Israeli wakainuka, wakakwea kwenda Betheli, nao wakataka shauri kwa Mungu; wakasema, Ni nani atakayekwea kwenda vitani kwanza kwa ajili yetu juu ya wana wa Benyamini? Bwana akawaambia, Yuda atakwea kwanza. 19 Basi wana wa Israeli waliondoka asubuhi, wakapanga hema zao juu ya Gibea. 20 Watu wa Israeli walitoka ili wapigane na Benyamini; nao watu wa Israeli wakaviandaa vita juu yao huko Gibea. 21 Wana wa Benyamini wakatoka Gibea, wakaangamiza hata nchi watu ishirini na mbili elfu katika Israeli siku hiyo. 22 Lakini watu hao, watu wa Israeli, walijitia nguvu, wakaviandaa vile vita mara ya pili mahali pale walipojiandaa siku ya kwanza. 23 Wana wa Israeli wakakwea juu na kulia mbele za Bwana hata jioni; wakamwuliza Bwana, wakisema, Je! Niende nikaribie tena kupiga vita juu ya wana wa Benyamini ndugu yangu? Bwana akasema, Haya, kweeni, mwende kupigana naye. 24 Basi wana wa Israeli wakakaribia juu ya wana wa Benyamini siku ya pili. 25 Benyamini alitoka kupigana nao kutoka Gibea siku ya pili, wakaangamiza hata nchi watu kumi na nane elfu tena katika watu wa Israeli; hao wote walikuwa wenye kutumia upanga. 26 Ndipo wana Israeli wote, na hao watu wote, wakakwea, wakaenda Betheli, na kulia, wakaketi hapo mbele za Bwana, wakafunga siku hiyo hata jioni; nao wakasongeza sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani mbele za Bwana. 27 Kisha wana wa Israeli wakauliza kwa Bwana (kwa sababu sanduku la agano la Mungu lilikuwako huko siku hizo, 28 na Finehasi, mwana wa Eleazari, mwana wa Haruni, alikuwa anasimama mbele ya hilo sanduku siku hizo), wakasema, Je! Nitoke tena niende kupigana na wana wa Benyamini ndugu yangu, au niache? Bwana akawaambia, Haya, kweeni; kwa kuwa kesho nitamtoa na kumtia mkononi mwako. 29 Basi Israeli akaweka watu wavizie kinyume cha Gibea kuuzunguka pande zote. 30 Basi wana wa Israeli wakakwea kwenda kupigana na wana wa Benyamini siku ya tatu, wakajipanga ili kupigana na Gibea, kama walivyofanya nyakati nyingine. 31 Nao wana wa Benyamini wakatoka waende kupigana nao, wakavutwa waende mbali na huo mji; kisha wakaanza kupiga na kuua katika hao watu, wapata kama watu thelathini wa Israeli, kama walivyofanya nyakati nyingine, katika hizo njia kuu, ambazo njia mojawapo huendelea Betheli, na njia ya pili huendelea Gibea, katika shamba. 32 Wana wa Benyamini wakasema, Wamepigwa mbele yetu kama kwanza. Lakini wana wa Israeli wakasema, Haya, na tukimbie, na kuwavuta wauache mji waende katika njia kuu. 33 Basi hao watu wote wa Israeli wakaondoka mahali pao wakajipanga huko Baal-tamari; na hao wenye kuvizia wa Israeli wakatoka mahali hapo walipokuwa, hata Maare-geba. 34 Kisha watu elfu kumi waliochaguliwa katika Israeli wote wakaja juu ya Gibea, na vile vita vilikuwa vikali sana; lakini hawakujua ya kuwa uovu ulikuwa karibu nao. 35 Bwana akampiga Benyamini mbele ya Israeli; na wana wa Israeli waliangamiza watu waume ishirini na tano elfu na mia moja, wa Benyamini siku hiyo; wote hao waliokuwa wenye kutumia upanga. 36 Basi wana wa Benyamini waliona kuwa wamepigwa; kwa kuwa watu wa Israeli wakaondoka mbele ya Benyamini, kwa sababu walikuwa wanawatumaini hao wenye kuvizia waliokuwa wamewaweka kinyume cha Gibea. 37 Hao wenye kuvizia wakafanya haraka, wakaurukia Gibea; na hao wenye kuvizia wakaenda wakaupiga huo mji wote kwa makali ya upanga. 38 Basi hiyo ishara iliyoaganwa kati ya watu wa Israeli na hao wenye kuvizia ilikuwa ni hii, kwamba wafanye lipande wingu kubwa la moshi kutoka katika huo mji. 39 Nao watu wa Israeli walipogeuka katika vile vita, Benyamini naye akaanza kupiga na kuwaua watu wa Israeli kama watu thelathini; kwani walisema, Hakika yetu wamepigwa mbele yetu, vile vile kama katika vile vita vya kwanza. 40 Lakini hapo hilo wingu lilipoanza kupanda kutoka katika mji, kama nguzo ya moshi, ndipo Wabenyamini wakaangalia nyuma, na tazama, huo mji mzima ulikuwa wapaa juu katika moshi kwenda mbinguni. 41 Ndipo watu wa Israeli wakageuka, na watu wa Benyamini walisitushwa; kwa kuwa waliona ya kwamba wamefikiliwa na uovu. 42 Kwa hiyo wakageuza maungo yao mbele ya wana wa Israeli kuelekea njia ya kwenda nyikani; lakini vile vita vikawaandamia kwa kasi; na hao waliotoka katika ile miji wakawaangamiza katikati yake. 43 Waliwazingira Wabenyamini pande zote na kuwafukuza, na kuwakanyaga-kanyaga hapo walipopumzika, hata kufikilia Gibea upande wa maawio ya jua. 44 Wakaanguka watu wa Benyamini watu kumi na nane elfu, hao wote walikuwa ni watu waume mashujaa. 45 Kisha wakageuka na kukimbia upande wa nyika hata kulifikilia jabali la Rimoni; nao wakaokota katika watu hao katika njia kuu watu waume elfu tano; wakawaandamia kwa kasi mpaka Gidomu, nako wakawapiga wengine wao watu elfu mbili. 46 Basi jumla ya watu wa Benyamini walioanguka siku ile walikuwa ni watu ishirini na tano elfu waliokuwa wanatumia upanga; wote hao walikuwa ni watu mashujaa. 47 Lakini watu waume mia sita wakageuka, wakakimbia upande wa nyikani mpaka jabali la Rimoni, wakakaa kwenye hilo jabali la Rimoni muda wa miezi minne. 48 Kisha watu wa Israeli wakageuka tena kuwaendea wana wa Benyamini, wakawapiga kwa makali ya upanga, huo mji mzima, na hao wanyama wa mji, na kila kitu walichokiona; tena miji yote waliyoiona wakaitia moto.

Waamuzi 21

1 Basi watu wa Israeli walikuwa wameapa huko katika Mispa, wakisema, Hapana mtu awaye yote kwetu sisi atakayemwoza binti yake kumpa Benyamini. 2 Basi hao watu wakafikilia Betheli, wakaketi kuko mbele ya Mungu hata jioni, nao wakainua sauti zao na kulia sana. 3 Wakasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, kwani jambo hili kuwa katika Israeli, ya kwamba hivi leo ni kabila moja limepunguka katika Israeli? 4 Kisha ikawa siku ya pili yake, hao watu wakaamka asubuhi na mapema, wakajenga madhabahu huko, wakasongeza sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. 5 Wana wa Israeli wakasema, Katika hizi kabila zote za Israeli ni ipi isiyofika katika mkutano kumkaribia Bwana? Kwa maana walikuwa wameweka kiapo kikuu katika habari za huyo asiyefika kumkaribia Bwana huko Mispa, huku wakisema, Hakika yake atauawa huyo. 6 Nao wana wa Israeli wakaghairi kwa ajili ya ndugu yao Benyamini, wakasema, Kabila moja imekatiliwa mbali na Israeli hivi leo. 7 Tufanyeje sisi ili tuwapatie wake hao waliosalia, kwa kuwa tumeapa kwa Bwana ya kwamba hatutawapa binti zetu ili wawaoe? 8 Basi wakasema, Ni ipi katika kabila za Israeli ambayo haikufika mbele ya Bwana huko Mispa? Na tazama, hakuja mmoja maragoni aliyetoka Yabeshi gileadi aufikilie huo mkutano. 9 Kwa maana hapo watu walipohesabiwa, hakuwapo hata mtu mmoja katika wenyeji wa Yabesh-gileadi. 10 Basi mkutano walipeleka huko watu kumi na mbili elfu wa hao waliokuwa mashujaa sana, kisha wakawaamuru, wakisema, Endeni mkawapige wenyeji wa Yabesh-gileadi kwa makali ya upanga, na hata wanawake na watoto wadogo. 11 Na jambo mtakalotenda ni hili; mtamwangamiza kila mume kabisa, na kila mwanamke ambaye amelala na mume. 12 Nao wakapata katika wenyeji wa Yabesh-gileadi wanawali mia nne, ambao hawajamjua mtu mume kwa kulala naye; basi wakawaleta maragoni huko Shilo, ulioko katika nchi ya Kanaani. 13 Basi mkutano ukatuma watu na kunena na wana wa Benyamini waliokuwako huko katika jabali la Rimoni, wakawatangazia amani. 14 Basi Benyamini wakarudi wakati huo; nao wakawapa wale wanawake waliowaponya wali hai katika hao wanawake wa Yabesh-gileadi; lakini hawakuwatosha. 15 Nao watu wakaghairi kwa ajili ya Benyamini, kwa sababu Bwana alikuwa amefanya pengo katika hizo kabila za Israeli. 16 Ndipo hao wazee wa huo mkutano walisema, Je! Tufanyeje ili tuwapatie wake hao waliosalia, kwa kuwa wanawake wameangamizwa katika Benyamini? 17 Wakasema, Lazima kuwa urithi kwa hao wa Benyamini waliopona, isiwe kabila kufutika katika Israeli. 18 Lakini sisi hatuwezi kuwaoza binti zetu kwa maana wana wa Israeli walikuwa wameapa, wakisema, Na alaaniwe huyo atakayempa Benyamini mke. 19 Kisha wakasema, Angalieni, iko sikukuu ya Bwana mwaka baada ya mwaka katika Shilo, ulioko upande kaskazini wa Betheli, upande wa mashariki wa hiyo njia kuu iendeayo kutoka Betheli kwenda Shekemu, nao ni upande wa kusini wa Lebona. 20 Basi wakawaagiza hao wana wa Benyamini wakisema, Haya, endeni, mkaotee katika mashamba ya mizabibu, 21 mkaangalie, kisha tazameni, kwamba hao binti za Shilo watoka ili wacheze katika hiyo michezo, basi tokeni ninyi mizabibuni, nanyi kila mtu na amshike mkewe katika hao binti za Shilo, kisha rudini nchi ya Benyamini. 22 Kisha itakuwa, hapo baba zao au ndugu zao, watakapokuja kushitaki, sisi tutawaambia, Kwa ihisani yenu tupeni sisi; kwa kuwa hatukumtwalia kila mtu mkewe katika vita; wala ninyi hamkuwapa wao, au kama sivyo ninyi sasa mngekuwa na hatia. 23 Wana wa Benyamini wakafanya vivyo, wakajitwalia wake, sawasawa na hesabu yao, katika hao waliocheza, wakawachukua wakaenda nao; kisha wakaenda kuurudia urithi wao, na kuijenga miji na kuikaa. 24 Nao wana wa Israeli wakati huo wakaenda zao, kila mtu akaenda kwa kabila yake na kwa jamaa yake; nao wakatoka huko, waende kila mtu kuuendea urithi wake. 25 Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; kila mtu alifanya yaliyokuwa ni mema machoni pake mwenyewe.

Ruthu 1

1 Ikawa zamani za Waamuzi walipoamua, kulikuwa na njaa katika nchi. Akaondoka mtu mmoja wa Bethlehemu ya Yuda, akaenda kukaa katika nchi ya Moabu, yeye na mkewe na wanawe wawili. 2 Na jina la mtu huyo aliitwa Elimeleki, na jina la mkewe Naomi, na majina ya wanawe wawili Maloni na Kilioni, Waefrathi wa Bethlehemu ya Yuda. Wakafika nchi ya Moabu, wakakaa huko. 3 Akafa Elimeleki, mumewe Naomi; na yule mwanamke akasalia na wanawe wawili. 4 Nao wakaoa wake katika wanawake wa Moabu; na jina la mmoja aliitwa Orpa, na jina la wa pili Ruthuu. Wakakaa huko yapata miaka kumi. 5 Wakafa na Maloni na Kilioni wote wawili; na huyo mwanamke akawa amefiwa na wanawe wawili, na mumewe pia. 6 Ndipo alipoondoka, yeye na wakweze, ili kurudi kutoka nchi ya Moabu; maana huko katika nchi ya Moabu amesikia ya kwamba Bwana amewajilia watu wake na kuwapa chakula. 7 Basi akatoka pale alipokuwapo, na wakweze wawili pamoja naye; wakashika njia ili kurudi mpaka nchi ya Yuda. 8 Kisha Naomi akawaambia wakweze wawili, Nendeni sasa mkarejee kila mmoja nyumbani kwa mamaye; Bwana na awatendee mema ninyi, kama ninyi mlivyowatendea mema hao waliofariki na mimi pia. 9 Bwana na awajalie kuona raha kila mmoja nyumbani kwa mumewe. Kisha akawabusu; nao wakapaza sauti zao wakalia. 10 Wakamwambia, La, sivyo; lakini tutarudi pamoja nawe kwa watu wako. 11 Naye Naomi akasema, Enyi wanangu, mrejee; kwani kufuatana na mimi? Je! Mimi ninao watoto wa kiume tena tumboni mwangu, hata wawe waume zenu? 12 Enyi wanangu, mrejee; nendeni zenu; kwa kuwa mimi ni mzee, siwezi kupata mume tena. Kama ningesema, Natumaini; kama ningepata mume hata usiku huu, na kuzaa watoto wa kiume; 13 je! Mngesubiri hata watakapokuwa watu wazima? Mngejizuia msiwe na waume? La, sivyo, wanangu; maana ni vigumu kwangu kuliko kwenu, kwa sababu mkono wa Bwana umetoka juu yangu. 14 Nao wakapaza sauti zao, wakalia tena, na Orpa akambusu mkwewe, lakini Ruthuu akaambatana naye. 15 Naye akasema, Tazama, shemeji yako amerejea kwa watu wake, na kwa mungu wake; basi urejee wewe umfuate shemeji yako. 16 Naye Ruthuu akasema, Usinisihi nikuache, Nirejee nisifuatane nawe; Maana wewe uendako nitakwenda, Na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, Na Mungu wako atakuwa Mungu wangu; 17 Pale utakapokufa nitakufa nami, Na papo hapo nitazikwa; Bwana anitende vivyo na kuzidi, Ila kufa tu kutatutenga wewe nami. 18 Basi alipomwona kuwa amekaza nia yake kufuatana naye, aliacha kusema naye. 19 Hivyo hao wakaendelea wote wawili hata walipofika Bethlehemu. Na ikawa walipofika Bethlehemu, mji wote ulitaharuki kwa habari zao. Nao wanawake wakasema, Je! Huyu ni Naomi? 20 Akawaambia, Msiniite Naomi niiteni Mara,kwa sababu Mwenyezi Mungu amenitenda mambo machungu sana. 21 Mimi nalitoka hali nimejaa, naye Bwana amenirudisha sina kitu, kwani kuniita Naomi, ikiwa Bwana ameshuhudia juu yangu, na Mwenyezi Mungu amenitesa? 22 Basi Naomi akarudi; pamoja na Ruthuu Mmoabi, mkwewe; ambao walirudi kutoka nchi ya Moabu; nao wakafika Bethlehemu mwanzo wa mavuno ya shayiri.

Ruthu 2

1 Basi huyo Naomi alikuwa na ndugu ya mumewe, mtu mkuu mwenye mali, wa jamaa yake Elimeleki, na jina lake aliitwa Boazi. 2 Naye Ruthuu Mmoabi akamwambia Naomi, Sasa niende kondeni, niokote masazo ya masuke nyuma yake yule ambaye nitaona kibali machoni pake. Akamwambia, Haya, mwanangu, nenda. 3 Basi akaenda, akaja akaokota masazo kondeni nyuma ya wavunaji; na bahati yake ikamtukia kwamba akaifika sehemu ya shamba iliyokuwa mali yake huyo Boazi, ambaye alikuwa wa jamaa yake Elimeleki. 4 Na tazama, Boazi akaja kutoka Bethlehemu kawaamkia wavunaji, akasema, Bwana akae nanyi. Nao wakamwitikia, Bwana na akubariki. 5 Kisha Boazi akamwuliza mtumishi aliyewasimamia wavunaji, Na huyu je! Ni msichana wa nani? 6 Yule msimamizi aliyewasimamia wavunaji akajibu, akasema, Ni yule msichana Mmoabi aliyerudi pamoja na Naomi, kutoka nchi ya Moabu; 7 naye akasema, Tafadhali niruhusu kuokota masazo, na kukusanya nyuma ya wavunaji kati ya miganda; basi akaja, naye ameshinda tangu asubuhi hata sasa, isipokuwa alikaa nyumbani kitambo kidogo. 8 Basi Boazi akamwambia Ruthuu, Mwanangu, sikiliza; wewe usiende kuokota masazo katika shamba lingine, wala usiondoke hapa, lakini ukae papa hapa karibu na wasichana wangu. 9 Macho yako na yaelekee konde walivunalo, ufuatane nao; je! Sikuwaagiza vijana wasikuguse? Tena, ukiona kiu, uende kwenye vyombo, nawe uyanywe waliyoyateka hao vijana. 10 Ndipo aliposujudia, akainama mpaka nchi, akamwambia, Jinsi gani nimepata kibali machoni pako, hata ukanifahamu, mimi niliye mgeni? 11 Naye Boazi akajibu, akamwambia, Nimeelezwa sana yote uliyomfanyia mkweo, tangu alipokufa mumeo; na jinsi ulivyowaacha baba yako na mama yako, na nchi yako uliyozaliwa, ukawafikilia watu usiowajua tangu hapo. 12 Bwana akujazi kwa kazi yako, nawe upewe thawabu kamili na Bwana, Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kukimbilia chini ya mabawa yake. 13 Ndipo aliposema, Bwana wangu, na nipate kibali machoni pako; kwa sababu wewe umeniburudisha moyo, na kumwambia mema mjakazi wako, ingawa mimi si kama mmojawapo wa wajakazi wako. 14 Tena wakati wa chakula huyo Boazi akamwambia, Karibu kwetu, ule katika mkate wetu, na ulichovye tonge lako katika siki yetu. Basi akaketi pamoja na wavunaji, nao wakampitishia bisi, naye akala akashiba, hata akasaza. 15 Naye alipoinuka tena ili aende kuokota masazo, huyo Boazi aliwaagiza vijana wake akisema, Mwacheni aokote hata kati ya miganda, wala msimkemee. 16 Tena mtoleeni kidogo katika matita na kukiacha, na akiokote, wala msimkataze. 17 Basi Ruthuu akaokota masazo kondeni hata jioni; kisha akazipura zile nafaka alizoziokota, zikawa yapata efa moja ya shayiri. 18 Akajitwika, akaenda zake mjini. Akamwonyesha mkwewe zile alizoziokota; akavitoa vile vyakula alivyovisaza alipokwisha kushiba, akampa. 19 Basi mkwewe akamwuliza, Je! Umeokota wapi leo? Umefanya kazi wapi? Na abarikiwe yeye aliyekufahamu. Naye akamwarifu mkwewe ni nani ambaye alifanya kazi kwake, akasema, Yule mtu niliyefanya kazi kwake leo jina lake aitwa Boazi. 20 Naye Naomi akamwambia mkwewe, Na abarikiwe huyo na Bwana, ambaye hakuuacha wema wake, wala kwa hao walio hai wala kwao waliokufa. Kisha Naomi akamwambia, Mtu huyu ni wa mbari yetu, mmojawapo wa jamaa yetu aliye karibu. 21 Naye Ruthuu Mmoabi akasema, Naam, akaniambia, Ukae papa hapa karibu na vijana wangu, hata watakapomaliza mavuno yangu yote. 22 Kisha Naomi akamwambia Ruthuu mkwewe, Mwanangu, ni vizuri wewe ufuatane na wasichana wake, wala watu wasikukute katika konde linginelo lote. 23 Hivyo yeye akafuatana na wasichana wake Boazi na kuokota, hata mwisho wa mavuno ya shayiri na mavuno ya ngano pia; naye alikuwa akikaa kwa mkwewe.

Ruthu 3

1 Kisha Naomi akamwambia mkwewe, Je! Mwanangu, si vizuri nikutafutie raha, ili upate mema? 2 Basi na huyu Boazi, je! Siye wa mbari yetu, ambaye ulikuwapo pamoja na wasichana wake? Tazama, usiku wa leo atakuwa akipepeta shayiri pale ugani. 3 Basi wewe oga, ujipake mafuta ujivike mavazi yako, kisha uende kwenye uga; walakini usijionyeshe kwake mtu yule, ila atakapokwisha kula na kunywa. 4 Nayo itakuwa wakati atakapolala, utapaangalia mahali alalapo, nawe uingie, uifunue miguu yake ujilaze hapo; na yeye atakuambia utakalofanya. 5 Akamwambia, Hayo yote unenayo mimi nitayafanya. 6 Basi akashuka mpaka ugani; akafanya yote kama vile mkwewe alivyomwagiza. 7 Ikawa huyo Boazi alipokwisha kula na kunywa, na moyo wake umekunjuka, alikwenda kulala penye mwisho wa chungu ya nafaka; na huyo mwanamke akaja taratibu, akaifunua miguu yake, akajilaza papo hapo. 8 Na ikawa usiku wa manane yule mtu akasituka, akajigeuza; na kumbe! Yupo mwanamke amelala miguuni pake. 9 Akasema, Ama! Ni nani wewe? Akamjibu, Ni mimi, Ruthuu, mjakazi wako; uitande nguo yako juu ya mjakazi wako; kwa kuwa ndiwe wa jamaa aliye karibu. 10 Akamwambia, Mwanangu, ubarikiwe na Bwana; umezidi kuonyesha fadhili zako mwisho kuliko mwanzo, kwa vile usivyowafuata vijana, kama ni maskini kama ni matajiri. 11 Basi, mwanangu, usiogope; mimi nitakufanyia yote uyanenayo; kwa maana mji wote pia wa watu wangu wanakujua ya kwamba u mwanamke mwema. 12 Tena ndiyo kweli ya kuwa mimi ni wa jamaa yako aliye karibu; lakini kuna mtu wa jamaa aliye karibu kuliko mimi. 13 Wewe ungoje usiku huu; kisha, asubuhi, kama akikubali kukufanyia impasavyo jamaa, haya, na akufanyie; lakini ikiwa hataki yeye, basi mimi nitakufanyia impasavyo jamaa; Bwana aishivyo. Ulale wewe hata asubuhi. 14 Hivyo huyo mwanamke akalala miguuni pake hata asubuhi; akaondoka mapema asijaweza mtu kumtambua mwenziwe; maana Boazi amesema, Isijulikane kabisa ya kuwa mwanamke alifika penye uga. 15 Tena alisema, Lete hapa shela yako uliyoivaa, uishike; naye akaishika; naye akampimia vipimo sita vya shayiri akamtwika; kisha huyo mwanamke akaenda zake mjini. 16 Basi alipofika kwa mkwewe, huyo akamwuliza, Je! Mwanangu, imekuwaje? Akamwambia yote yule mtu aliyomfanyia. 17 Akasema, Na vipimo hivi sita vya shayiri amenipa; maana akaniambia, Usiende kwa mkweo mikono mitupu. 18 Naye mkwewe akasema, Basi, mwanangu, tulia; hata utakapojua jinsi litakavyotukia jambo hili; kwa sababu mtu huyu hataridhika, asipolimaliza jambo hilo leo.

Ruthu 4

1 Basi Boazi akakwea kwenda mpaka langoni, akaketi pale; na tazama, yule mtu wa jamaa aliyekuwa karibu, ambaye Boazi amemnena, akapita. Naye akamwita, Haya! Wewe, karibu, uketi hapa. Naye akaja akaketi. 2 Kisha akatwaa watu kumi miongoni mwa wazee wa mji, akawaambia, Ninyi nanyi, ketini hapa. Wakaketi. 3 Kisha akamwambia yule jamaa, Huyu Naomi, aliyerudi hapa kutoka nchi ya Moabu, anauza sehemu ya ardhi aliyokuwa nayo ndugu yetu, Elimeleki; 4 nami ilikuwa nia yangu nikujulishe wewe, na kukuambia, Uinunue mbele ya hawa waliopo na mbele ya wazee wa watu wangu. Kama wewe utaikomboa, haya, uikomboe; lakini kama hutaikomboa, uniambie ili nijue mimi; kwa kuwa hakuna mtu wa kuikomboa ila wewe, na baada yako ni mimi. Naye akasema, Nitaikomboa mimi. 5 Ndipo Boazi aliposema, Siku ile utakapolinunua shamba mkononi mwa Naomi, unamnunua Ruthuu pia, huyu Mmoabi, mkewe marehemu, ili makusudi umwinulie marehemu jina katika urithi wake. 6 Basi yule jamaa aliyekuwa wa karibu akasema, Mimi sitaweza kulikomboa kwa nafsi yangu, nisije nikauharibu urithi wangu mwenyewe; basi haki yangu ya kulikomboa ujichukulie wewe, maana mimi sitaweza kulikomboa. 7 Basi hii ilikuwa desturi zamani za kale katika Israeli, kwa habari ya kukomboa na kubadiliana, ili kuyahakikisha yote; mtu huvua kiatu chake na kumpa mwenziwe; ndivyo walivyohakikisha neno katika Israeli. 8 Basi yule jamaa akamwambia Boazi, Wewe ujinunulie mwenyewe. Akavua kiatu chake. 9 Naye Boazi akawaambia wale wazee na watu wote, Leo hivi ninyi ni mashahidi ya kwamba mimi nimenunua yote yaliyokuwa ya Elimeleki, na yote yaliyokuwa ya Kilioni na Maloni, mkononi mwa Naomi. 10 Tena, huyu Ruthuu Mmoabi, mkewe Maloni, nimemnunua awe mke wangu, makusudi nipate kumwinulia marehemu jina katika urithi wake, jina lake marehemu lisikatike miongoni mwa ndugu zake, wala langoni pa mji wake; leo hivi ninyi ni mashahidi. 11 Na watu wote waliokuwapo langoni, na wale wazee, wakasema, Naam, sisi ni mashahidi. Bwana na amfanye mwanamke huyu aingiaye nyumbani mwako kuwa kama Raheli na kama Lea, wale wawili walioijenga nyumba ya Israeli. Nawe ufanikiwe katika Efrata, na kuwa mashuhuri katika Bethlehemu. 12 Nyumba yako na ifanane na nyumba yake Peresi, ambaye kwamba Tamari alimzalia Yuda, kwa wazao atakaokupa Bwana katika mwanamke huyu. 13 Basi Boazi akamtwaa Ruthuu, naye akawa mke wake; naye akaingia kwake, na Bwana akamjalia kuchukua mimba, naye akazaa mtoto wa kiume. 14 Nao wale wanawake wakamwambia Naomi, Na ahimidiwe Bwana, asiyekuacha leo hali huna wa jamaa aliye karibu; jina lake huyu na liwe kuu katika Israeli. 15 Naye atakurejezea uhai wako, na kukuangalia katika uzee wako; kwa maana mkweo, ambaye akupenda, naye anakufaa kuliko watoto saba, ndiye aliyemzaa. 16 Basi Naomi akamtwaa yule mtoto, akamweka kifuani pake, akawa mlezi wake. 17 Nao wale wanawake waliokuwa jirani zake wakampa jina, wakisema, Naomi amezaliwa mwana; wakamwita jina lake Obedi; yeye ndiye baba yake Yese, aliye baba yake Daudi. 18 Hivi ndivyo vizazi vya Peresi; Peresi alimzaa Hesroni; 19 na Hesroni akamzaa Ramu; na Ramu akamzaa Aminadabu; 20 na Aminadabu akamzaa Nashoni; na Nashoni akamzaa Salmoni; 21 na Salmoni akamzaa Boazi; na Boazi akamzaa Obedi; 22 na Obedi akamzaa Yese; na Yese akamzaa Daudi.

1 Samweli 1

1 Palikuwa na mtu mmoja wa Rama, Msufi, wa nchi ya milima milima ya Efraimu, jina lake akiitwa Elkana, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu, mwana wa Sufu, Mwefraimu 2 naye alikuwa na wake wawili; jina lake mmoja akiitwa Hana, na jina lake wa pili aliitwa Penina; naye huyo Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakuwa na watoto. 3 Na mtu huyo alikuwa akikwea kutoka mjini kwake mwaka kwa mwaka, ili kuabudu, na kumtolea Bwana wa majeshi dhabihu katika Shilo. Na wale wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi, makuhani wa Bwana, walikuwako huko. 4 Hata siku ile ilipofika Elkana alipotoa dhabihu, kumpa mkewe Penina sehemu, akawapa na watoto wake wote, waume kwa wake, sehemu zao; 5 lakini Hana humpa sehemu mara mbili; maana alimpenda Hana, ingawa Bwana alikuwa amemfunga tumbo. 6 Ila mwenzake humchokoza sana, hata kumsikitisha, kwa sababu Bwana alikuwa amemfunga tumbo. 7 Tena mumewe akafanya hivyo mwaka kwa mwaka, hapo yule mwanamke alipokwea kwenda nyumbani kwa Bwana, ndivyo yule alivyomchokoza; basi, kwa hiyo, yeye akalia, asile chakula. 8 Elkana mumewe akamwambia, Hana, unalilia nini? Kwani huli chakula? Kwa nini moyo wako una huzuni? Je! Mimi si bora kwako kuliko watoto kumi? 9 Ndipo Hana akainuka, walipokwisha kula na kunywa huko Shilo. Naye Eli, kuhani, alikuwa akiketi kitini pake penye mwimo wa hekalu la Bwana. 10 Naye huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni mwake, akamwomba Bwana akalia sana. 11 Akaweka nadhiri, akasema, Ee Bwana wa majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa Bwana huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe hautamfikilia kichwani kamwe. 12 Ikawa, hapo alipodumu kuomba mbele za Bwana, Eli akamwangalia kinywa chake. 13 Basi Hana alikuwa akinena moyoni mwake; midomo yake tu ilionekana kama anena, sauti yake isisikiwe; kwa hiyo huyo Eli alimdhania kuwa amelewa. 14 Ndipo Eli akamwambia, Je! Utakuwa mlevi hata lini? Achilia mbali divai yako. 15 Hana akajibu, akasema, Hasha! Bwana wangu, mimi ni mwanamke mwenye roho ya huzuni, mimi sikunywa divai wala kileo, ila nimeimimina roho yangu mbele za Bwana. 16 Usimdhanie mjakazi wako kuwa ni mwanamke asiyefaa kitu; kwa kuwa katika wingi wa kuugua kwangu na kusikitika kwangu ndivyo nilivyonena hata sasa. 17 Ndipo Eli akajibu, akasema, Enenda kwa amani; na Mungu wa Israeli akujalie haja yako uliyomwomba. 18 Naye akasema, Mjakazi wako na aone kibali machoni pako. Basi huyo mwanamke akaenda zake, naye akala chakula, wala uso wake haukukunjamana tena. 19 Wakaondoka asubuhi na mapema, wakasali mbele za Bwana, kisha wakarejea na kufika nyumbani kwao huko Rama; Elkana akamjua mkewe Hana; naye Bwana akamkumbuka. 20 Ikawa, wakati ulipowadia, Hana akachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; akamwita jina lake Samweli, akisema, Kwa kuwa nimemwomba kwa Bwana. 21 Kisha yule mtu, Elkana, na watu wote wa nyumbani mwake, wakakwea kwenda kumtolea Bwana dhabihu ya mwaka, na nadhiri yake. 22 Bali Hana hakukwea; maana alimwambia mumewe, Sitakwea mimi hata mtoto wangu atakapoachishwa maziwa, hapo ndipo nitakapomleta, ili ahudhurie mbele za Bwana, akae huko daima. 23 Elkana, mumewe, akamwambia, Haya, fanya uonavyo vema; ngoja hata utakapomwachisha maziwa; Bwana na alithibitishe neno lake tu. Basi yule mwanamke akangoja, akamnyonyesha mtoto wake, hata akamwachisha maziwa. 24 Naye alipokuwa amekwisha kumwachisha maziwa, akamchukua pamoja naye, na ng'ombe watatu, na efa moja ya unga,na chupa ya divai,akamleta nyumbani kwa BWANA,huko Shilo ;na Yule mtoto alikuwa mtoto mdogo. 25 Nao wakamchinja huyo ng'ombe, wakamleta mtoto kwa Eli. 26 Akasema, Ee bwana wangu, kama iishivyo roho yako, bwana wangu, mimi ndimi yule mwanamke aliyesimama karibu nawe hapa, nikimwomba Bwana. 27 Naliomba nipewe mtoto huyu; Bwana akanipa dua yangu niliyomwomba; 28 kwa sababu hiyo mimi nami nimempa Bwana mtoto huyu; wakati wote atakaokuwa hai amepewa Bwana. Naye akamwabudu Bwana huko.

1 Samweli 2

1 Naye Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka katika Bwana, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia wokovu wako; 2 Hakuna aliye mtakatifu kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna mwamba kama Mungu wetu. 3 Msizidi kunena kwa kutakabari hivyo; Majivuno yasitoke vinywani mwenu; Kwa kuwa Bwana ni Mungu wa maarifa, Na matendo hupimwa na yeye kwa mizani. 4 Pinde zao mashujaa zimevunjika, Na hao waliojikwaa wamefungiwa nguvu. 5 Walioshiba wamejikodisha ili kupata chakula, Na hao waliokuwa na njaa wamepata raha. Naam, huyo aliyekua tasa amezaa watoto saba, Na yeye aliye na wana wengi amedhoofika. 6 Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. 7 Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. 8 Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake. 9 Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; 10 Washindanao na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake. 11 Kisha Elkana akaenda Rama nyumbani kwake. Na yule mtoto akamtumikia Bwana mbele yake Eli, kuhani. 12 Basi, hao wana wa Eli walikuwa watu wasiofaa kitu; hawakumjali Bwana, 13 wala haki ya makuhani ilivyokuwa kwa watu. Wakati huo mtu ye yote alipotoa dhabihu wakati wo wote, ndipo huja mtumishi wa kuhani, nyama ilipokuwa katika kutokota, naye akawa na uma wa meno matatu mkononi mwake; 14 naye huutia kwa nguvu humo chunguni, au birikani, au sufuriani, au chomboni; nyama yote iliyoinuliwa kwa huo uma kuhani huichukua mwenyewe. Ndivyo walivyofanya huko Shilo kwa Waisraeli wote waliokuja huko. 15 Tena, kabla ya kuteketeza mafuta, huja mtumishi wa kuhani, akamwambia yule mwenye kuitoa dhabihu, Mtolee kuhani nyama ya kuoka; kwa kuwa hataki kupewa nyama iliyotokoswa, bali nyama mbichi. 16 Tena, ikiwa mtu yule amwambia, Hawakosi wataichoma moto hayo mafuta kwanza, kisha utwae kadiri roho yako itakavyopenda; ndipo husema, Sivyo, lakini sharti unipe sasa hivi; la, hunipi, basi nitaitwaa kwa nguvu. 17 Hivyo dhambi yao wale vijana ilikuwa kubwa sana machoni pa Bwana; kwa maana hao watu walidharau sadaka ya Bwana. 18 Lakini Samweli alikuwa akitumika mbele za Bwana, naye alikuwa kijana, mwenye kuvaa naivera ya kitani. 19 Tena mamaye humfanyizia kanzu ndogo, na kumletea mwaka kwa mwaka, hapo alipokwea pamoja na mumewe ili kutoa dhabihu kila mwaka. 20 Naye Eli akambariki Elkana na mkewe, akasema, Bwana na akupe uzao kwa mwanamke huyu, badala ya azimo aliloazimiwa Bwana. Kisha wakaenda nyumbani kwao. 21 Naye Bwana akamwangalia Hana, naye akachukua mimba, akazaa watoto, wa kiume watatu na wa kike wawili. Naye huyo mtoto Samweli akakua mbele za Bwana. 22 Basi Eli alikuwa mzee sana; naye alisikia habari za mambo yote ambayo wanawe waliwatenda Waisraeli; na jinsi walivyolala na wanawake waliokuwa wakitumika mlangoni pa hema ya kukutania. 23 Akawaambia, Mbona mnatenda mambo kama hayo? Maana nasikia habari za matendo yenu mabaya kwa watu hawa wote. 24 Sivyo hivyo, wanangu, kwa maana habari hii ninayoisikia si habari njema; mnawakosesha watu wa Bwana. 25 Mtu mmoja akimkosa mwenzake, Mungu atamhukumu; lakini mtu akimkosa Bwana, ni nani atakayemtetea? Lakini hawakuisikia sauti ya baba yao, kwa sababu Bwana amekusudia kuwaua. 26 Na yule mtoto, Samweli, akazidi kukua akapata kibali kwa Bwana, na kwa watu pia. 27 Kisha mtu wa Mungu akamwendea Eli, akamwambia, Bwana asema hivi, Je! Mimi sikujidhihirisha nafsi yangu kwa nyumba ya baba yako, walipokuwa katika Misri, wakiitumikia nyumba ya Farao? 28 Je! Sikumchagua yeye katika kabila zote za Israeli, ili awe kuhani wangu, apande madhabahuni kwangu; na kufukiza uvumba, na kuvaa naivera mbele zangu? Nami sikuwapa watu wa mbari ya baba yako dhabihu zote za wana wa Israeli zilizotolewa kwa moto? 29 Kwa nini basi mnaipiga teke dhabihu yangu na sadaka yangu nilizoziamuru katika maskani yangu; ukawaheshimu wanao kuliko mimi, mpate kujinenepesha kwa sadaka zote za watu wangu Israeli zilizo njema? 30 Kwa sababu hiyo, Bwana, Mungu wa Israeli, asema, Ni kweli, nalisema ya kuwa nyumba yako, na nyumba ya baba yako itakwenda mbele zangu milele; lakini sasa Bwana asema, Jambo hili na liwe mbali nami; kwa maana wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu. 31 Angalia, siku zinakuja, nitakapoukata mkono wako, na mkono wa mbari ya baba yako, hata nyumbani mwako hatakuwako mzee. 32 Nawe utalitazama teso la maskani yangu, katika utajiri wote watakaopewa Israeli; wala nyumbani mwako hatakuwako mzee milele. 33 Tena mtu wa kwako, ambaye sitamtenga na madhabahu yangu, atakuwa mtu wa kukupofusha macho, na kukuhuzunisha moyo; tena wazao wote wa nyumba yako watakufa wapatapo kuwa watu wazima. 34 Na hii ndiyo ishara itakayokuwa kwako, itakayowapata wana wako wawili, Hofni na Finehasi; watakufa wote wawili katika siku moja. 35 Nami nitajiinulia kuhani mwaminifu, atakayefanya sawasawa na mambo yote niliyo nayo katika moyo wangu, na katika nia yangu; nami nitamjengea nyumba iliyo imara; naye atakwenda mbele ya masihi wangu milele. 36 Kisha itakuwa, ya kwamba kila mtu atakayesalia katika nyumba yako atakwenda kumsujudia, apate kipande kidogo cha fedha, na mkate mmoja; na kumwambia, Tafadhali unitie katika kazi mojawapo ya ukuhani, nipate kula kipande kidogo cha mkate.

1 Samweli 3

1 Basi, mtoto Samweli akamtumikia Bwana mbele ya Eli. Na neno la Bwana lilikuwa adimu siku zile; hapakuwa na mafunuo dhahiri. 2 Ikawa wakati huo, Eli alipokuwa amelala mahali pake (tena macho yake yalikuwa yameanza kupofuka, hata asiweze kuona), 3 na taa ya Mungu ilikuwa haijazimika bado, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu la Bwana, palipokuwa na sanduku la Mungu; 4 basi, wakati huo Bwana akamwita Samweli; naye akasema, Mimi hapa. 5 Akamwendea Eli kwa haraka, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akasema, Sikukuita; kalale tena. Naye akaenda, akalala tena. 6 Bwana akaita mara ya pili, Samweli! Samweli! Akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akajibu, Sikukuita, mwanangu; kalale tena. 7 Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. 8 Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto. 9 Kwa hivyo Eli akamwambia Samweli, Enenda, kalale; itakuwa, akikuita, utasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. Basi Samweli akaenda akalala mahali pake. 10 Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. 11 Bwana akamwambia Samweli, Angalia, nitatenda tendo katika Israeli, ambalo kila atakayelisikia masikio yake yatamwasha. 12 Siku hiyo nitayatimiza maneno yale yote niliyoyasema juu ya Eli katika habari za nyumba yake, tangu mwanzo hata mwisho. 13 Kwa maana nimemwambia ya kwamba nitaihukumu nyumba yake milele, kwa ajili ya ule uovu alioujua; kwa kuwa wanawe walijiletea laana, wala yeye hakuwazuia. 14 Na kwa hiyo nimeapa juu ya nyumba ya Eli, ya kwamba uovu wa nyumba ya Eli hautasafika kwa dhabihu wala kwa sadaka hata milele. 15 Naye Samweli akalala hata asubuhi, akaifungua milango ya nyumba ya Bwana. Samweli akaogopa kumjulisha Eli maono hayo. 16 Basi Eli akamwita Samweli, akasema, Samweli, mwanangu. Naye akajibu, Mimi hapa. 17 Akamwuliza, Ni neno gani alilosema nawe? Nakusihi, usinifiche; Mungu akufanyie vivyo hivyo, na kuzidi, ukinificha lo lote katika hayo yote Bwana aliyosema nawe. 18 Basi Samweli akamwambia kila neno, asimfiche lo lote. Naye akasema, Ndiye Bwana; na afanye alionalo kuwa ni jema. 19 Samweli akakua, naye Bwana alikuwa pamoja naye, wala hakuliacha neno lake lo lote lianguke chini. 20 Nao Waisraeli wote, toka Dani mpaka Beer-sheba, walitambua ya kwamba huyo Samweli amewekwa kuwa nabii wa Bwana. 21 Naye Bwana akaonekana tena huko Shilo; kwa kuwa Bwana akajifunua kwa Samweli huko Shilo, kwa neno la Bwana. Nalo neno la Samweli likawajia Israeli wote.

1 Samweli 4

1 [Ikawa siku zile Wafilisti walikusanyika ili kupigana na Israeli,] nao Waisraeli wakatoka juu ya Wafilisti kwenda vitani;wakatua karibu na Ebenezeri ,nao Wafilisti wakatua huko Afeki. 2 Nao Wafilisti wakajipanga juu ya Israeli; na walipopigana, Israeli wakapigwa mbele ya Wafilisti; wakauawa watu wa jeshi lao lililokuwa uwandani wapata watu elfu nne. 3 Hata watu walipofika kambini, wazee wa Israeli wakasema, Mbona Bwana ametupiga leo mbele ya Wafilisti? Twende tukalilete sanduku la agano la Bwana toka Shilo hata huku, lije kati yetu, na kutuokoa katika mikono ya adui zetu. 4 Basi wakatuma watu kwenda Shilo, nao wakalileta toka huko sanduku la agano la Bwana wa majeshi, akaaye juu ya makerubi; na Hofni na Finehasi, wana wawili wa Eli, walikuwako huko pamoja na sanduku la agano la Mungu. 5 Na sanduku la agano la Bwana lilipoingia kambini, Israeli wote wakapiga kelele kwa sauti kuu, hata nchi ikavuma. 6 Nao Wafilisti waliposikia mshindo wa zile kelele, walisema, Maana yake nini mshindo wa kelele hizi kubwa katika kambi ya Waebrania? Wakatambua ya kuwa sanduku la Bwana limefika kambini. 7 Wafilisti wakaogopa, maana walisema, Mungu ameingia kambini. Wakasema, Ole wetu! Kwani halijawa jambo kama hili tangu hapo. 8 Ole wetu! Ni nani atakayetuokoa na mkono wa miungu hawa walio hodari? Hawa ndio miungu waliowapiga Wamisri kwa mapigo ya kila namna jangwani. 9 Iweni hodari, na kufanya kiume enyi Wafilisti, msije mkawa watumwa wa Waebrania, kama wao walivyokuwa watumwa wenu; fanyeni kiume, mkapigane nao. 10 Wafilisti wakapigana nao, Israeli wakapigwa, wakakimbia kila mtu hemani kwake; wakauawa watu wengi sana; maana katika Israeli walianguka watu thelathini elfu wenye kwenda vitani kwa miguu. 11 Hilo sanduku la Mungu Likatwaliwa; na Hofni na Finehasi, wale wana wawili wa Eli, wakauawa. 12 Basi, mtu mmoja wa Benyamini akapiga mbio kutoka mle jeshini akafika Shilo siku ile ile, hali nguo zake zimeraruliwa, na mavumbi kichwani mwake. 13 Alipofika, tazama, Eli alikuwa ameketi kitini pake kando ya njia, akingojea; maana moyo wake ulitetemeka kwa ajili ya sanduku la Mungu. Na yule mtu alipoingia mjini, akatoa habari, mji wote ukalia. 14 Naye Eli aliposikia kelele za kile kilio, akasema, Maana yake nini kelele za kishindo hiki? Yule mtu akafanya haraka, akaenda, akamwambia Eli. 15 Basi Eli umri wake umepata miaka tisini na minane; na macho yake yamepofuka hata asiweze kuona. 16 Yule mtu akamwambia Eli, Mimi ndimi niliyetoka jeshini, nami leo hivi nimekimbia toka jeshini. Naye akasema, Yalikwendaje, mwanangu? 17 Yeye aliyeleta habari akajibu, akasema, Israeli wamekimbia mbele ya Wafilisti, tena watu wengi sana wameuawa, hata na wana wako wawili, Hofni na Finehasi, wamekufa pia, na sanduku la Mungu limetwaliwa. 18 Ikawa alipolitaja sanduku la Mungu, Eli akaanguka kitini pake kwa nyuma, kando ya mlango, shingo yake ikavunjika, akafa; maana alikuwa mzee, tena mzito. Naye alikuwa amewaamua Israeli miaka arobaini. 19 Tena mkwewe, mkewe huyo Finehasi, alikuwa mja-mzito, karibu na kuzaa; basi, aliposikia habari ya kutwaliwa sanduku la Mungu, na ya kwamba mkwewe na mumewe wamekufa, akajiinamisha, akazaa; maana utungu wake ulimfikilia. 20 Hata alipokuwa katika kufa, wale wanawake waliohudhuria karibu naye wakamwambia, Usiogope; kwa maana umezaa mtoto mwanamume. Walakini hakujibu, wala hakumtazama. 21 Akamwita mtoto, Ikabodi, akisema, Huo utukufu umeondoka katika Israeli; kwa sababu sanduku la Mungu lilikuwa limetwaliwa, na kwa sababu ya mkwewe na mumewe. 22 Naam, akasema, Huo utukufu umeondoka katika Israeli; maana sanduku la Mungu limetwaliwa. Print this page Top WordProject - "Hapo mwanzo kulikuwako Neno ..." - Contact * * * * * * *

1 Samweli 5

1 Basi Wafilisti walikuwa wamelichukua sanduku la Mungu, wakaenda nalo kutoka Eben-ezeri hata Ashdodi. 2 Wafilisti wakalichukua sanduku la Mungu, wakalitia katika nyumba ya Dagoni, wakaliweka karibu na Dagoni. 3 Na watu wa Ashdodi, walipoamka alfajiri siku ya pili, kumbe! Dagoni imeanguka chini kifudifudi, mbele ya sanduku la Bwana. Wakaitwaa Dagoni, wakaisimamisha mahali pake tena. 4 Hata walipoamka kesho yake asubuhi, kumbe! Dagoni ilikuwa imeanguka chini kifudifudi, mbele ya sanduku la Bwana; na kichwa chake Dagoni na vitanga vya mikono yake vyote viwili vimekatika, vipo vimelala kizingitini; Dagoni ikasalia kiwiliwili chake tu. 5 Kwa hiyo makuhani wa Dagoni, na mtu awaye yote aingiaye nyumbani mwa Dagoni, hawakanyagi kizingiti cha nyumba ya Dagoni huko Ashdodi, hata leo. 6 Lakini mkono wa Bwana ulikuwa mzito juu ya watu wa Ashdodi, akawaharibu, akawapiga kwa majipu, huko Ashdodi na mipakani mwake. 7 Kisha hao watu wa Ashdodi, walipoona ilivyokuwa, walisema, Hilo sanduku la Mungu wa Israeli halitakaa kwetu; kwa maana mkono wake ni mzito juu yetu, na juu ya Dagoni, mungu wetu. 8 Basi wakatuma watu waende kuwakusanya kwao mashehe wote wa Wafilisti, wakasema, Tulifanyieje sanduku la Mungu wa Israeli? Nao wakajibu, Sanduku la Mungu wa Israeli na lihamishwe liende Gathi. Wakalihamisha sanduku la Mungu wa Israeli. 9 Ikawa, walipokwisha lihamisha, mkono wa Bwana ulikuwa juu ya mji huo, kwa kuwafadhaisha sana; akawapiga watu wa mjini, wadogo kwa wakubwa, wakapatwa na majipu. 10 Basi, wakalipeleka sanduku la Mungu mpaka Ekroni. Ikawa, sanduku la Mungu lilipofika Ekroni, watu wa Ekroni walifanya kelele, wakasema, Wamelileta hilo sanduku la Mungu wa Israeli kwetu, hata kutuua sisi na watu wetu. 11 Kwa hiyo wakatuma watu waende kuwakusanya mashehe wote wa Wafilisti, wakasema, Liondoeni hilo sanduku la Mungu wa Israeli, liende tena mahali pake, ili lisituue sisi, wala watu wetu; kwa sababu kulikuwa na fadhaa kubwa sana mjini mwote; mkono wa Mungu ulikuwa mzito mno huko. 12 Na wale wasiokufa walipigwa kwa yale majipu; na kilio cha mji kikafika mbinguni.

1 Samweli 6

1 Basi, hilo sanduku la Bwana lilikuwamo katika nchi ya Wafilisti muda wa miezi saba. 2 Nao Wafilisti wakawaita makuhani na waaguzi, wakasema, Tulifanyieje sanduku la Bwana? Tuonyesheni jinsi tuwezavyo kulirudisha mahali pake. 3 Nao wakajibu, Mkilirudisha hilo sanduku la Mungu wa Israeli, msilirudishe kitupu; lakini msikose kumpelekea na matoleo ya kosa; hivyo mtapona, tena mtafunuliwa ni kwa sababu gani mkono wake haukuondolewa kwenu. 4 Ndipo wakauliza, Na hayo matoleo ya kosa yatakuwa ya namna gani, hayo tutakayompelekea? Nao wakajibu, Na yawe majipu ya dhahabu matano, na panya wa dhahabu watano, sawasawa na idadi ya mashehe wa Wafilisti; kwa kuwa tauni moja ilikuwa juu yenu nyote, na juu ya mashehe wenu. 5 Kwa hiyo mtafanyiza sanamu za majipu yenu, na sanamu za panya wenu waiharibuo nchi; nanyi mtamtukuza huyo Mungu wa Israeli; huenda ataupunguza uzito wa mkono wake juu yenu, na juu ya miungu yenu, na juu ya nchi yenu. 6 Mbona, basi, mnaifanya migumu mioyo yenu, kama vile wale Wamisri, naye yule Farao, walivyoifanya migumu mioyo yao? Hata na hao, hapo alipokwisha kuwadhihaki, je! Hawakuwaruhusu watu, nao wakaenda zao? 7 Basi sasa jifanyizieni gari jipya, mtwae na ng'ombe wake wawili wakamwao, ambao hawajafungwa nira, nanyi mkawafunge hao ng'ombe garini, na kuwaondoa ndama zao na kuwatia zizini; 8 kisha, litwaeni hilo sanduku la Bwana, na kuliweka juu ya gari; na hivyo vitu vya dhahabu, mtakavyompelekea kuwa matoleo ya kosa, mvitie katika kasha kando yake; mkalipeleke sanduku, lipate kwenda. 9 Kisha angalieni, likikwea kwa njia ya mpakani mwake kwenda Beth-shemeshi, basi, ndiye aliyetutenda uovu huo mkuu; la, sivyo, ndipo tutakapojua ya kwamba si mkono wake uliotupiga; ilikuwa ni ajali iliyotupata. 10 Basi watu wale walifanya hivyo; wakatwaa ng'ombe wawili wakamwao, wakawafunga garini, na ndama zao wakawafunga zizini; 11 kisha wakaliweka sanduku la Bwana juu ya gari, pamoja na kasha lenye panya wa dhahabu na sanamu za majipu yao. 12 Na hao ng'ombe wakashika njia moja kwa moja kwenda Beth-shemeshi; wakaiandama njia ya barabara, wakaenda wakilia, lakini hawakugeukia upande wa kuume wala wa kushoto; na mashehe wa Wafilisti wakawafuata hata kuufikia mpaka wa Beth-shemeshi. 13 Nao watu wa Beth-shemeshi walikuwa wakivuna ngano yao bondeni; wakainua macho yao, wakaliona sanduku, wakafurahi sana kuliona. 14 Na lile gari likaingia katika konde la Yoshua wa Beth-shemeshi, na kusimama pale pale, palipokuwapo jiwe kubwa; basi wakaipasua miti ya lile gari, wakawatoa wale ng'ombe kuwa ni sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana. 15 Nao Walawi walilishusha sanduku la Bwana, na lile kasha lililokuwa pamoja nalo, lenye vile vitu vya dhahabu; wakaviweka juu ya lile jiwe kubwa; nao watu wa Beth-shemeshi wakatoa sadaka za kuteketezwa, na kuchinja dhabihu siku iyo hiyo kwa Bwana. 16 Na hao mashehe watano wa Wafilisti, hapo walipokwisha kuyaona hayo, walirejea Ekroni siku iyo hiyo. 17 Hii ndiyo hesabu ya yale majipu waliyoyapeleka wale Wafilisti, yawe matoleo ya kosa kwa Bwana; kwa Ashdodi moja, kwa Gaza moja, kwa Ashkeloni moja, kwa Gathi moja, na kwa Ekroni moja; 18 na panya wa dhahabu, kwa idadi ya miji yote ya Wafilisti, milki zao wale mashehe watano, miji yenye maboma na vijiji vya mashamba pia. Nalo lile jiwe kubwa, ambalo juu yake waliliweka sanduku la Bwana, liko hata hivi leo hapo kondeni pa Yoshua wa Beth-shemeshi. 19 Basi Bwana aliwapiga baadhi ya watu wa Beth-shemeshi, kwa sababu wamechungulia ndani ya hilo sanduku la Bwana, wapata watu sabini, na watu hamsini elfu; nao watu wakalalamika, kwa kuwa Bwana amewapiga watu kwa uuaji mkuu. 20 Nao watu wa Beth-shemeshi wakasema, Ni nani awezaye kusimama mbele za Bwana, huyu Mungu mtakatifu? Naye atapanda kwenda kwa nani kutoka kwetu? 21 Nao wakatuma wajumbe waende kwa wenyeji wa Kiriath-yearimu, kusema, Wafilisti wamelirudisha sanduku la Bwana; basi shukeni, mkalichukue kwenu.

1 Samweli 7

1 Na hao watu wa Kiriath-yearimu wakaja, wakalichukua sanduku la Bwana, wakalileta ndani ya nyumba ya Abinadabu huko kilimani, nao wakamtenga Eleazari, mwanawe, ili alilinde sanduku la Bwana. 2 Ikawa, tangu siku hiyo ambayo sanduku lilikaa Kiriath-yearimu wakati ulikuwa mwingi; kwa maana ulikuwa miaka ishirini; na nyumba yote ya Israeli wakamwombolezea Bwana. 3 Basi Samweli akawaambia nyumba yote ya Israeli, akasema, Ikiwa mnamrudia Bwana kwa mioyo yenu yote, basi, iondoleeni mbali miungu migeni, nayo Maashtorethi yatoke kwenu, mkamtengenezee Bwana mioyo yenu, mkamtumikie yeye peke yake; naye atawaokoa katika mikono ya Wafilisti. 4 Ndipo wana wa Israeli wakayaondoa Mabaali na Maashtorethi, wakamtumikia Bwana peke yake. 5 Samweli akasema, Wakusanyeni Israeli wote Mispa, nami nitawaombea ninyi kwa Bwana. 6 Wakakusanyika huko Mispa, wakateka maji na kuyamimina mbele za Bwana; wakafunga siku ile, wakasema huko, Tumemfanyia Bwana dhambi. Samweli akawaamua wana wa Israeli huko Mispa. 7 Hata Wafilisti waliposikia ya kuwa wana wa Israeli wamekusanyika huko Mispa, mashehe wa Wafilisti walipanda juu ili kupigana na Israeli. Nao wana wa Israeli waliposikia, wakawaogopa Wafilisti. 8 Wana wa Israeli wakamwambia Samweli, Usiache kumlilia Bwana, Mungu wetu, kwa ajili yetu, kwamba atuokoe na mikono ya Wafilisti. 9 Ndipo Samweli akatwaa mwana-kondoo mchanga, akamtolea Bwana sadaka ya kuteketezwa nzima; Samweli akamlilia Bwana kwa ajili ya Israeli; Bwana akamwitikia. 10 Hata Samweli alipokuwa akiitoa hiyo sadaka ya kuteketezwa, Wafilisti wakakaribia ili kupigana na Israeli; walakini Bwana akapiga ngurumo, mshindo mkubwa sana, juu ya Wafilisti siku ile, akawafadhaisha; nao wakaangamizwa mbele ya Israeli. 11 Nao watu wa Israeli wakatoka Mispa, wakawafuatia Wafilisti, wakawapiga, hata walipofika chini ya Beth-kari. 12 Ndipo Samweli akatwaa jiwe, na kulisimamisha kati ya Mispa na Sheni, akaliita jina lake Eben-ezeri, akisema, Hata sasa Bwana ametusaidia. 13 Hivyo Wafilisti walishindwa, wasiingie tena ndani ya mipaka ya Israeli; na mkono wa Bwana ulikuwa juu ya Wafilisti siku zote za Samweli. 14 Nayo miji ile Wafilisti waliyokuwa wamewapokonya Waisraeli ilirudishwa tena kwa Israeli, tokea Ekroni mpaka Gathi; na Waisraeli wakauokoa mpaka wake mikononi mwa Wafilisti. Tena kulikuwa na amani kati ya Israeli na Waamori. 15 Naye huyo Samweli akawaamua Israeli siku zote za maisha yake. 16 Naye huenda mwaka kwa mwaka kuzunguka mpaka Betheli, na Gilgali, na Mispa; akawaamua Israeli mahali hapo pote. 17 Na kurudi kwake kulikuwa mpaka Rama; maana ndipo ilipokuwa nyumba yake; nako ndiko alikowaamua Israeli; na huko akamjengea Bwana madhabahu.

1 Samweli 8

1 Hata Samweli alipokuwa mzee, aliwafanya wanawe wawe waamuzi juu ya Israeli. 2 Na jina la mwanawe mzaliwa wa kwanza aliitwa Yoeli; na jina la wa pili Abiya; walikuwa waamuzi katika Beer-sheba. 3 Ila wanawe hawakuenda katika njia zake, bali waliziacha, ili wapate faida; wakapokea rushwa, na kupotosha hukumu. 4 Ndipo wazee wote wa Israeli wakakutana pamoja, wakamwendea Samweli huko Rama; 5 wakamwambia, Angalia, wewe umekuwa mzee, na wanao hawaendi katika njia zako; basi, tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote. 6 Lakini neno hilo likawa baya machoni pa Samweli, waliposema, Tupe mfalme atuamue. Naye Samweli akamwomba Bwana. 7 Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti ya watu hawa katika kila neno watakalokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao. 8 Kwa kadiri ya matendo yote waliyonitenda tokea siku ile nilipowatoa katika Misri hata leo, kwa kuniacha mimi, na kwa kutumikia miungu mingine, ndivyo wanavyokutenda wewe. 9 Basi sasa, isikilize sauti yao; walakini, uwaonye sana, na kuwaonyesha desturi ya mfalme atakayewamiliki. 10 Naye Samweli akawaambia wale watu waliotaka mfalme maneno yote ya Bwana. 11 Akasema, Mfalme atakayewamiliki ninyi atakuwa na desturi hii; atatwaa wana wenu na kuwaweka kwake, kwa magari yake, na kuwa wapanda farasi wake; nao watapiga mbio mbele ya magari yake. 12 Naye atawaweka kwake kuwa maakida juu ya elfu, na maakida juu ya hamsini; na wengine atawaweka walime shamba lake, na kuvuna mavuno yake, na kufanyiza zana zake za vita, na vyombo vya magari yake. 13 Na binti zenu atawatwaa kuwa wafanyaji wa marhamu, na wapishi, na waokaji. 14 Atatwaa makonde yenu, na mashamba yenu ya mizabibu, na ya mizeituni, yale yaliyo mazuri sana, ili awape watumishi wake. 15 Naye atawatoza ushuru wa mbegu zenu na wa mizabibu yenu, awape maakida wake, na watumishi Wake. 16 Atawatwaa watumishi wenu na wajakazi wenu, na ng'ombe zenu walio wazuri sana, na punda zenu, naye atawatia katika kazi zake mwenyewe. 17 Atawatoza fungu la kumi la makundi yenu; nanyi mtakuwa watumwa wake. 18 Nanyi mtalia siku ile kwa sababu ya mfalme wenu mliyejichagulia; Bwana asiwajibu siku ile. 19 Walakini hao watu wakakataa kuisikiliza sauti ya Samweli; wakasema, Sivyo hivyo; lakini tunataka kuwa na mfalme juu yetu; 20 ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu. 21 Samweli akayasikia maneno yote ya watu, akayanena masikioni mwa Bwana. 22 Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti yao, ukawafanyie mfalme. Kisha Samweli akawaambia watu wa Israeli, Enendeni kila mtu mjini kwake.

1 Samweli 9

1 Basi, kulikuwa na mtu mmoja wa Benyamini, jina lake akiitwa Kishi, mwana wa Abieli, mwana wa Serori, mwana wa Bekorathi, mwana wa Afia, mwana wa Mbenyamini, mtu shujaa, mwenye nguvu. 2 Naye alikuwa na mwana, aliyeitwa jina lake Sauli, kijana, tena mzuri; wala katika wana wa Israeli hakuwako mtu mzuri kuliko yeye; tangu mabega yake kwenda juu alikuwa mrefu kuliko watu wote. 3 Na punda za Kishi, baba yake Sauli, walikuwa wamepotea. Kishi akamwambia Sauli mwanawe, Haya basi, twaa mtumishi mmoja pamoja nawe, uondoke, uende ukawatafute punda hao. 4 Naye akapita kati ya nchi ya milima milima ya Efraimu, akapita na kati ya nchi ya Shalisha, lakini hawakuwaona; kisha wakapita kati ya nchi ya Shaalimu, wala huko hawakuwako; wakapita kati ya nchi ya Wabenyamini, lakini hawakuwapata. 5 Hata walipofika nchi ya Sufu, Sauli akamwambia yule mtumishi aliyefuatana naye, Haya, na turudi, baba yangu asije akaacha kufikiri habari za punda akatufikiri sisi. 6 Naye akamwambia, Tazama, katika mji huu mna mtu wa Mungu, naye ni mtu mwenye kuheshimiwa; yote asemayo hutukia kweli kweli; basi, twende huko; labda yeye aweza kutuambia habari ya safari yetu tunayoiendea. 7 Ndipo Sauli akamwambia mtumishi wake, Lakini angalia, kama tukienda, tumpelekee mtu huyo kitu gani? Maana chakula kimekwisha vyomboni mwetu, wala hapana zawadi ya kumpelekea mtu wa Mungu; tuna nini sisi? 8 Yule mtumishi akamjibu Sauli, akasema, Tazama, mkononi mwangu nina robo ya shekeli ya fedha; nitampa huyo mtu wa Mungu fedha hiyo, atuambie njia yetu. 9 (Hapo zamani katika Israeli, mtu alipokwenda kuuliza neno kwa Mungu, husema hivi, Haya! Twende kwa mwonaji; maana mtu aitwaye sasa Nabii hapo zamani aliitwa Mwonaji.) 10 Basi Sauli akamwambia mtumishi wake, Umesema vema; haya! Twende. Wakaenda mpaka mji ule aliokuwamo mtu wa Mungu. 11 Hata walipokwea kwenda mjini, wakakutana na wasichana, wanatoka kwenda kuteka maji; wakawaambia, Je! Mwonaji yuko? 12 Nao wakawajibu, wakasema, Yuko; tazama, yuko huko mbele yako; fanyeni haraka sasa, maana hivi leo amekuja mjini; kwa sababu watu wana dhabihu leo katika mahali pa juu; 13 mkiingia mjini tu, mara mtamwona, kabla hajakwea kwenda mahali pa juu ale chakula; maana, watu hawatakula hata yeye atakapokuja; kwa sababu yeye ndiye anayeibarikia dhabihu; kisha hao watu walioalikwa hula. Basi, kweeni sasa; maana wakati huu ndio mtakapomwona. 14 Nao wakakwea kwenda mjini; nao walipokuwa wakiingia mjini, tazama, Samweli akawatokea, kwenda mahali pa juu. 15 Basi Bwana alikuwa amemfunulia Samweli, siku moja kabla Sauli hajamwendea, akisema, 16 Kesho, wakati kama huu, nitakuletea mtu kutoka nchi ya Benyamini, nawe mtie mafuta ili awe mkuu juu ya watu wangu Israeli, naye atawaokoa watu wangu na mikono ya Wafilisti; maana nimewaangalia watu wangu, kwa sababu kilio chao kimenifikilia. 17 Hata Samweli alipomwona Sauli, Bwana akamwambia, Huyu ndiye niliyekuambia habari zake; huyu ndiye atakayewamiliki watu wangu. 18 Ndipo Sauli akamkaribia Samweli langoni, akasema, Tafadhali, uniambie, nyumba ya mwonaji iko wapi? 19 Samweli akamjibu Sauli, akasema, Mimi ndimi mwonaji; tangulia mbele yangu ukwee mpaka mahali pa juu, kwa maana mtakula pamoja nami leo; kisha, asubuhi nitakuacha uende zako, nami nitakuambia yote uliyo nayo moyoni mwako. 20 Na wale punda zako waliopotea siku hizi tatu, usijiudhi kwa ajili yao; maana wameonekana. Na yote yaliyotamanika katika Israeli amewekewa nani? Si wewe, na nyumba yote ya baba yako? 21 Basi Sauli akajibu, akasema, Je! Mimi si Mbenyamini, mtu wa kabila iliyo ndogo kuliko kabila zote za Israeli? Na jamaa yangu nayo si ndogo kuliko jamaa zote za kabila ya Benyamini? Kwa nini basi, kuniambia hivyo? 22 Naye Samweli akamtwaa Sauli na mtumishi wake, akawaleta ndani sebuleni, akawaketisha mahali pa heshima kati ya watu walioalikwa, nao jumla yao walikuwa kama watu thelathini. 23 Samweli akamwambia mpishi, Lete ile sehemu niliyokupa, hiyo niliyokuambia, Iweke akiba. 24 Basi mpishi akatwaa paja, na nyama iliyokuwa juu yake, akaiweka mbele ya Sauli. Samweli akasema, Iliyowekwa akiba ndiyo hiyo! Iweke mbele yako ule, kwa sababu umewekewa hiyo wewe hata wakati uliokusudiwa, maana nalisema, Nimewaalika watu. Basi Sauli akala pamoja na Samweli siku hiyo. 25 Hata waliposhuka kutoka mahali pa juu na kufika mjini, akaongea na Sauli darini. 26 Nao wakaamka alfajiri; kisha ikawa, kulipopambazuka, Samweli akamwita Sauli darini, akisema, Inuka, nikupeleke kwenu. Basi Sauli akainuka, nao wakatoka wote wawili, yeye na Samweli. 27 Hata walipokuwa wakishuka mwisho wa mji, Samweli akamwambia Sauli, Mwambie mtumishi atangulie, (naye akatangulia), bali wewe simama hapa sasa, ili nikuambie neno la Mungu.

1 Samweli 10

1 Ndipo Samweli akatwaa kichupa cha mafuta, akayamimina kichwani pake, akambusu, akasema, Je! Bwana hakukutia mafuta [uwe mkuu juu ya watu wake Israeli? Nawe utamiliki watu wa Bwana, na kuwaokoa na mikono ya adui zao; kisha hii itakuwa ishara kwako ya kuwa Bwana amekutia mafuta] uwe mkuu juu ya urithi wake. 2 Utakapoondoka kwangu leo, utakutana na wanaume wawili karibu na kaburi la Raheli, katika mpaka wa Benyamini huko Selsa; nao watakuambia, Punda hao uliokwenda kuwatafuta wameonekana; na tazama, baba yako ameacha kufikiri habari za punda, anafikiri habari zenu, akisema, Nifanye nini kwa ajili ya mwanangu? 3 Kisha utakwenda mbele kutoka hapo, na kufika kwa mwaloni wa Tabori, na hapo watu watatu watakutana nawe, wanaokwea kumwendea Mungu huko Betheli, mmoja anachukua wana-mbuzi watatu, na mwingine anachukua mikate mitatu, na mwingine anachukua kiriba cha divai; 4 nao watakusalimu na kukupa mikate miwili; nawe utaipokea mikononi mwao. 5 Baada ya hayo utafika Gibea ya Mungu, hapo palipo na ngome ya Wafilisti; kisha itakuwa, utakapofika mjini, utakutana na kundi la manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, wenye kinanda, na tari, na kinubi, na filimbi mbele yao, nao watakuwa wakitabiri; 6 na roho ya Bwana itakujilia kwa nguvu, nawe utatabiri pamoja nao, nawe utageuzwa kuwa mtu mwingine. 7 Basi, hapo ishara hizi zitakapokutukia, fanya kama uonavyo vema; kwa kuwa Mungu yu pamoja nawe. 8 Nawe utatelemka mbele yangu mpaka Gilgali; nami, angalia, nitakutelemkia huko, ili kutoa sadaka za kuteketezwa, na kuchinja sadaka za amani; siku saba utangoja, hata nitakapokujia, na kukuonyesha yatakayokupasa kuyafanya. 9 Ikawa, alipogeuka kumwacha Samweli, Mungu akambadilisha moyo; nazo ishara zile zote zikatukia siku ile ile. 10 Basi, walipofika Gibea, tazama, kikosi cha manabii wakakutana naye; kisha roho ya Mungu ikamjilia kwa nguvu, naye akatabiri kati yao. 11 Ikawa, wote waliomjua zamani walipoliona jambo hilo, kwamba, tazama, huyo anatabiri pamoja na manabii, ndipo watu wakasemezana, Ni nini hilo lililompata mwana wa Kishi? Je! Sauli pia yumo miongoni mwa manabii? 12 Naye akajibu mtu mmoja wa mahali hapo, akasema, Na baba yao n'nani? Kwa hiyo ikawa mithali, Je! Sauli pia yumo miongoni mwa manabii? 13 Naye alipokwisha kutabiri, alipafikilia mahali pale pa juu. 14 Basi babaye mdogo akamwuliza Sauli na mtumishi wake, Je! Mlikwenda wapi? Naye akajibu, Tulikwenda ili kuwatafuta hao punda; na tulipoona ya kwamba hawakuonekana, tulimwendea Samweli. 15 Babaye mdogo Sauli akasema, Tafadhali uniambie, huyo Samweli aliwaambiaje? 16 Lakini Sauli akamjibu babaye mdogo, Alituambia waziwazi ya kuwa hao punda wamekwisha onekana. Lakini habari ya ufalme, ambayo Samweli alimwambia, hakuitaja habari hiyo. 17 Basi Samweli akawakusanya watu mbele za Bwana huko Mispa 18 akawaambia wana wa Israeli, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Naliwatoa Israeli kutoka Misri, nami naliwaokoa ninyi na mikono ya Wamisri, na ya falme zote zilizowaonea; 19 lakini leo mmemkataa Mungu wenu, naye ndiye awaponyaye katika misiba yenu yote na shida zenu; nanyi mmemwambia, Sivyo, lakini weka mfalme juu yetu. Basi, sasa, hudhurieni mbele za Bwana, kwa kabila zenu na kwa elfu zenu. 20 Basi Samweli akawaleta kabila zote za Israeli karibu; na kabila ya Benyamini ikatwaliwa. 21 Kisha akaileta kabila ya Benyamini karibu, kwa jamaa zao; jamaa ya Wamatri ikatwaliwa. Akaileta jamaa ya Wamatri karibu, mtu baada ya mtu; kisha Sauli, mwana wa Kishi, akatwaliwa; lakini walipomtafuta hakuonekana. 22 Basi wakazidi kumwuliza Bwana, Amebaki mtu asiyekuja huku bado? Naye Bwana akajibu, Tazama, amejificha penye mizigo. 23 Basi wakaenda mbio wakamleta kutoka huko; naye aliposimama kati ya watu, alikuwa mrefu kuliko watu wote, tangu mabega yake kwenda juu. 24 Samweli akawaambia watu wote, Mnamwona mtu huyu aliyechaguliwa na Bwana, ya kuwa hakuna mtu mfano wake katika watu wote. Ndipo watu wote wakapiga kelele, wakasema, Mfalme na aishi! 25 Kisha Samweli aliwaambia watu madaraka ya ufalme, akayaandika katika kitabu, akakiweka mbele za Bwana. Samweli akawaruhusu watu wote, waende kila mtu nyumbani kwake. 26 Sauli naye akaenda nyumbani kwake huko Gibea; na pamoja naye wakaenda kikosi cha watu, ambao Mungu alikuwa ameigusa mioyo yao. 27 Walakini wengine wasiofaa kitu wakasema, Huyu je! Atatuokoaje? Nao wakamdharau, wasimletee zawadi.

1 Samweli 11

1 Ikawa, kama baada ya mwezi mmoja, Nahashi, Mwamoni ,akakwea na kupanga marago juu ya Yabesh-gileadi;na watu wote wa Yabeshi wakamwambia Nahashi, Fanya mapatano nasi,na sisi tutakutumikia. 2 Huyo Nahashi, Mwamoni, akawaambia, Kwa sharti hii mimi nitapatana nanyi, kila mtu ang'olewe jicho la kuume; na kwa jambo hilo nitawashutumu Waisraeli wote pia. 3 Basi wazee wa Yabeshi wakamjibu, Tuachie siku saba, ili tutume wajumbe waende mipakani mwote mwa Israeli; kisha, ikiwa hakuna atakayetuokoa, tutakutokea. 4 Hivyo wajumbe wakafika Gibea ya Sauli, wakasema maneno hayo masikioni mwa watu; na watu wote wakainua sauti zao wakalia. 5 Na tazama, Sauli akaja akifuata ng'ombe kutoka kondeni; naye Sauli akauliza, Watu hawa wana nini, hata wakalia? Wakamwambia maneno ya watu wale wa Yabeshi. 6 Na roho ya Mungu ikamjilia Sauli kwa nguvu, hapo alipoyasikia maneno yale, na hasira yake ikawaka sana. 7 Naye akatwaa jozi ya ng'ombe, akawakata-kata vipande, kisha akavipeleka vile vipande mipakani mwote mwa Israeli kwa mikono ya wajumbe, kusema, Ye yote asiyetoka nyuma ya Sauli na Samweli, ng'ombe zake watatendwa vivi hivi. Basi utisho wa Bwana ukawaangukia wale watu, wakatoka kama mtu mmoja. 8 Naye akawahesabu huko Bezeki; Waisraeli walikuwa mia tatu elfu, na Wayuda thelathini elfu. 9 Nao wakawaambia hao wajumbe waliokuja, Waambieni watu wa Yabesh-gileadi, Kesho, wakati wa jua kali, mtapata wokovu. Basi wale wajumbe wakaenda, wakawaarifu watu wa Yabeshi; nao walifurahiwa. 10 Kwa hiyo watu wa Yabeshi walisema, Kesho tutawatokea, nanyi mtatufanyia yote myaonayo kuwa ni mema. 11 Ikawa, kesho yake, Sauli akawapanga watu katika vikosi vitatu; nao wakaingia katikati ya marago kwenye zamu ya asubuhi, wakawapiga Waamoni hata wakati wa jua kali; kisha ikawa wale waliosalia wakatawanyika, hata wasiachwe wawili wao pamoja. 12 Ndipo watu walipomwambia Samweli, Ni nani yule aliyesema, Je! Huyo Sauli atatutawala? Walete watu hao, ili tuwaue. 13 Lakini Sauli akasema, Hakuna mtu atakayeuawa leo, maana leo Bwana amefanya wokovu katika Israeli. 14 Kisha Samweli akawaambia watu, Haya! Na twendeni mpaka Gilgali, ili tuuimarishe ufalme huko mara ya pili. 15 Nao watu wote wakaenda Gilgali; wakamtawaza Sauli mbele za Bwana huko Gilgali; wakachinja sadaka za amani mbele za Bwana; na huko Sauli na watu wote wa Israeli wakafurahi sana.

1 Samweli 12

1 Kisha Samweli akawaambia Israeli wote, Angalieni, nimeisikiliza sauti yenu katika hayo yote mliyoniambia, nami nimemtawaza mfalme juu yenu. 2 Basi sasa, angalieni, mfalme anakwenda mbele yenu; na mimi ni mzee, mwenye mvi; tena, tazameni, wana wangu wapo pamoja nanyi; nami nimekwenda mbele yenu toka ujana wangu hata leo. 3 Nami nipo hapa; basi, mnishuhudie mbele za Bwana, na mbele ya masihi wake,nalitwaa ng`ombe wa nani? au nalitwaa punda wa nani? au ni nani niliye mdhulumu? Ni nani niliyemwonea? Au kwa mkono wa nani nimepokea rushwa inipofushe macho? Nami nitawarudishia ninyi. 4 Nao wakasema, hukutudhulumu, wala hukutuonea, wala hukupokea kitu kwa mkono wa mtu awaye yote. 5 Akawaambia, Bwana ni shahidi juu yenu, na masihi 6 Samweli akawaambia watu, Ni yeye Bwana aliyewaweka Musa na Haruni, ndiye yeye aliyewatoa baba zenu kutoka nchi ya Misri. 7 Basi sasa simameni, ili niwahutubie mbele za Bwana, kwa kutaja matendo yote ya haki ya Bwana, aliyowatendea ninyi na baba zenu. 8 Yakobo alipokuwa ameingia Misri, na baba zenu walipomlilia Bwana, ndipo Bwana akawapeleka Musa na Haruni, nao wakawatoa baba zenu kutoka Misri, wakawakalisha mahali hapa. 9 Lakini wakamsahau Bwana, Mungu wao, naye akawauza na kuwatia katika mikono ya Sisera, jemadari wa jeshi la Hazori, na katika mikono ya Wafilisti, na katika mikono ya mfalme wa Moabu, nao wakapigana nao. 10 Nao wakamlilia Bwana, wakasema, Tumefanya dhambi, kwa kuwa tumemwacha Bwana, na kuwatumikia Mabaali na Maashtorethi; lakini sasa utuokoe na mikono ya adui zetu, nasi tutakutumikia wewe. 11 Bwana akawatuma Yerubaali, na Baraka, na Yeftha, na Samweli, akawaokoa ninyi na mikono ya adui zenu pande zote, nanyi mkakaa salama. 12 Hata mlipomwona Nahashi, mfalme wa wana wa Amoni, amekuja kupigana nanyi, mliniambia, Sivyo, lakini mfalme atatutawala; ingawa Bwana, Mungu wenu, ni mfalme wenu. 13 Basi sasa, mtazameni mfalme mliyemchagua na kumtaka; tazameni, Bwana ameweka mfalme juu yenu. 14 Kama mkimcha Bwana, na kumtumikia, na kuisikia sauti yake, msiiasi amri ya Bwana, tena kama ninyi, na mfalme anayewatawala, mkimfuata Bwana, Mungu wenu, vema! 15 Bali msipoisikia sauti ya Bwana, mkiiasi amri ya Bwana, ndipo mkono wa Bwana utakuwa juu yenu, kama ulivyokuwa juu ya baba zenu. 16 Na sasa simameni, mkalione jambo hili kubwa, Bwana atakalolitenda mbele ya macho yenu. 17 Leo je! Si mavuno ya ngano? Nitamwomba Bwana, kwamba apeleke ngurumo na mvua; nanyi mtajua na kuona ya kuwa uovu wenu ni mwingi sana, mlioufanya machoni pa Bwana, kwa kujitakia mfalme. 18 Basi Samweli akamwomba Bwana, naye Bwana akapeleka ngurumo na mvua siku ile; nao watu wote wakamwogopa Bwana sana, na Samweli pia. 19 Watu wote wakamwambia Samweli, Utuombee sisi watumwa wako kwa Bwana, Mungu wako, tusije tukafa; maana tumeongeza dhambi zetu zote kwa uovu huu, wa kujitakia mfalme. 20 Samweli akawaambia, Msiogope; ni kweli mmeutenda uovu huu wote; lakini msigeuke na kuacha kumfuata Bwana, bali mtumikieni Bwana kwa mioyo yenu yote. 21 Wala msigeuke upande, maana, kufuata vitu vya ubatili, 22 visivyoweza kusaidia wala kuokoa, kwa kuwa havifai kitu. Maana Bwana hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu; kwa kuwa imempendeza Bwana kuwafanya ninyi kuwa watu wake mwenyewe. 23 Walakini mimi, hasha! Nisimtende Bwana dhambi kwa kuacha kuwaombea ninyi; lakini nitawaelimisha katika njia iliyo njema, na kunyoka 24 Mcheni Bwana tu, mkamtumikie kwa kweli kwa mioyo yenu yote; maana, kumbukeni jinsi alivyowatendea mambo makuu. 25 Lakini kama mkiendelea kutenda mabaya, mtaangamia, ninyi na mfalme wenu pia.

1 Samweli 13

1 Sauli alikuwa na umri wa miaka kadha wa kadha hapo alipoanza kutawala;naye akatawala miaka kadha wa kadha juu ya Israeli. 2 Naye Sauli alijichagulia watu elfu tatu wa Israeli; ambao katika hao, elfu mbili walikuwa pamoja na Sauli katika Mikmashi, na katika mlima wa Betheli na elfu moja pamoja na Yonathani katika Gibea ya Benyamini; nao wale watu waliosalia akawaruhusu waende kila mtu hemani kwake. 3 Yonathani akaipiga hiyo ngome ya Wafilisti, iliyokuwako huko Gibea, nao Wafilisti wakapata habari. Naye Sauli akapiga tarumbeta katika nchi yote, huku akisema, Na wasikie Waebrania. 4 Waisraeli wote wakasikia habari ya kwamba Sauli ameipiga hiyo ngome ya Wafilisti, na ya kwamba Waisraeli wamepata kuwa makuruhi kwa Wafilisti. Basi hao watu wakakusanyika pamoja kumfuata Sauli huko Gilgali. 5 Nao Wafilisti wakakusanyana ili wapigane na Waisraeli, magari thelathini elfu, na wapanda farasi sita elfu, na watu kama mchanga ulio ufuoni mwa bahari kwa wingi wao; wakapanda juu, wakapiga kambi yao katika Mikmashi, upande wa mashariki wa Beth-aveni. 6 Hata Waisraeli walipoona ya kuwa wa katika dhiki, (maana watu walifadhaishwa), ndipo hao watu wakajificha katika mapango, na katika vichaka, na katika miamba, na katika mashimo, na katika mabirika. 7 Hata baadhi ya Waebrania walivuka Yordani, wakaingia nchi ya Gadi na Gileadi; lakini Sauli alikuwa akaliko huko Gilgali, nao watu wote wakamfuata wakitetemeka. 8 Akangoja siku saba, kwa kadiri ya muhula uliowekwa na Samweli lakini Samweli hakuja Gilgali; na hao watu wakatawanyika mbali naye. 9 Sauli akasema, Nileteeni hapa sadaka ya kuteketezwa na sadaka za amani. Akaitoa sadaka ya kuteketezwa. 10 Hata mara alipokwisha kuitoa hiyo sadaka ya kuteketezwa, kumbe! Samweli akatokea. Naye Sauli akatoka kwenda kumlaki na kumsalimu. 11 Samweli akasema, Umefanya nini? Naye Sauli akasema, Ni kwa sababu naliona ya kuwa watu wanatawanyika mbali nami, na wewe hukuja siku zile zilizonenwa; nao Wafilisti wamekusanyika pamoja huko Mikmashi; 12 basi nikasema, Wafilisti watanishukia sasa mpaka Gilgali, kabla sijaomba fadhili za Bwana; kwa hiyo nalijishurutisha, nikatoa sadaka ya kuteketezwa. 13 Naye Samweli akamwambia Sauli, Umefanya upumbavu; hukuishika amri ya Bwana, Mungu wako, aliyokuamuru; kwa maana Bwana angaliufanya ufalme wako kuwa imara juu ya Israeli milele. 14 Lakini sasa ufalme wako hautadumu; Bwana amejitafutia mtu aupendezaye moyo wake, naye Bwana amemwamuru yeye kuwa mkuu juu ya watu wake, kwa sababu wewe hukulishika neno lile Bwana alilokuamuru. 15 Basi Samweli akaondoka, akapanda kutoka Gilgali mpaka Gibea ya Benyamini. Naye Sauli akawahesabu watu waliokuwapo pamoja naye, wapata kama mia sita. 16 Naye Sauli, na mwanawe Yonathani, na watu waliokuwapo pamoja nao, wakakaa huko Geba ya Benyamini; lakini Wafilisti wakatua katika Mikmashi. 17 Nao watekaji wa nyara wakatoka katika marago ya hao Wafilisti, vikosi vitatu; kikosi kimoja kikageukia njia iendayo Ofra, mpaka nchi ya Shuali; 18 na kikosi kingine kikageukia njia iendayo Beth-horoni; na kikosi kingine kikageukia njia ya mpakani ielekeayo bonde la Seboimu upande wa nyika. 19 Basi, hakuonekana mhunzi ye yote katika nchi yote ya Israeli; kwa kuwa Wafilisti walisema, Waebrania wasije wakajifanyizia panga au mikuki; 20 lakini Waisraeli wote hushuka kwa Wafilisti, ili kunoa kila mtu jembe lake, na mundu wake, na shoka lake, na sululu yake; 21 ila walikuwa na tupa za kunolea sululu, na miundu, na mauma, na mashoka; na kwa kuinoa michokoo. 22 Hivyo ikawa, siku ya vita, haukuonekana mkononi mwa mtu ye yote, miongoni mwa watu waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani, upanga wala mkuki; isipokuwa Sauli mwenyewe na mwanawe Yonathani walikuwa navyo. 23 Na jeshi la Wafilisti wakatoka hata mwanya wa Mikmashi.

1 Samweli 14

1 Basi ikatukia siku moja, ya kwamba Yonathani, mwana wa Sauli, akamwambia yule kijana aliyemchukulia silaha zake, Haya! Na tuwavukie Wafilisti ngomeni, pale ng'ambo ya pili. Walakini hakumwarifu babaye. 2 Naye Sauli alikuwa akikaa katika upande wa mwisho wa Giba, chini ya mkomamanga ulioko kwenye uga; na hao watu waliokuwa pamoja naye walipata watu mia sita; 3 na Ahiya, mwana wa Ahitubu nduguye Ikabodi, mwana wa Finehasi, mwana wa Eli, kuhani wa Bwana huko Shilo, mwenye kuvaa naivera. Tena hao watu hawakujua ya kwamba Yonathani ameondoka. 4 Na katikati ya mianya, ambayo Yonathani alitaka kuipitia ili kuifikilia hiyo ngome ya Wafilisti, palikuwa na genge la jabali upande huu, na genge la jabali upande huu; jina la moja liliitwa Bosesi, na jina la pili Sene. 5 Hilo genge moja limesimama upande wa kaskazini, mbele ya Mikmashi, na hilo la pili upande wa kusini, mbele ya Geba. 6 Basi, Yonathani akamwambia yule kijana aliyemchukulia silaha zake, Haya! Na twende tukawavukie ngomeni hao wasiotahiriwa; yamkini Bwana atatutendea kazi; kwa maana hakuna la kumzuia Bwana asiokoe, kwamba ni kwa wengi au kwamba ni kwa wachache. 7 Naye huyo mchukua silaha akamjibu, Fanya yote yaliyomo moyoni mwako; angalia, mimi hapa ni pamoja nawe, moyo wangu ni kama moyo wako. 8 Ndipo Yonathani akasema, Tazama, sisi tutawavukia watu hawa, na kujidhihirisha kwao. 9 Nao wakituambia hivi, Ngojeni, hata sisi tuwafikilie; ndipo tusimame pale pale mahali petu, tusiwapandie. 10 Lakini wakisema hivi, Haya! Ninyi, tupandieni sisi; hapo ndipo tutakapopanda; kwa maana Bwana amewatia mikononi mwetu; na hii itakuwa ndiyo ishara kwetu. 11 Basi, hao wote wawili wakajidhihirisha mbele ya ngome ya Wafilisti, na wale Wafilisti wakasema, Kumbe! Wale Waebrania watoka katika mashimo walimojificha! 12 Nao watu wa ngomeni wakamjibu Yonathani na mchukua silaha zake, wakasema, Haya! Ninyi, pandeni juu hapa tulipo, na sisi tutawaonyesha jambo. Yonathani akamwambia yule aliyezichukua silaha, Haya! Panda nyuma yangu; kwa kuwa Bwana amewatia mikononi mwa Israeli. 13 Basi Yonathani akapanda kwa mikono na miguu yake, na mchukua silaha nyuma yake; na hao watu wakaanguka mbele ya Yonathani; na huyo mchukua silaha zake akawaua nyuma yake. 14 Na uuaji huo wa kwanza walioufanya Yonathani na mchukua silaha zake, ulipata kama watu ishirini, katika nafasi kama nusu ya kiwanja kiwezacho kulimwa katika siku nzima. 15 Kukawa na tetemeko katika marago, na katika mashamba, na katikati ya watu wote; watu wa ngomeni, na watekaji wa nyara, wakatetemeka nao; hata na nchi ikatetemeka pia; basi kulikuwa na tetemeko kubwa mno. 16 Nao wale walinzi wa Sauli huko Gibea ya Benyamini wakaangalia, na tazama, mkutano ule ulikuwa ukitoweka, na watu walikuwa wakienda huko na huko. 17 Ndipo Sauli akawaambia watu waliokuwa pamoja naye, Haya! Hesabuni sasa, mkaone ni nani aliyeondoka kwetu. Nao walipokwisha hesabu, tazama Yonathani na yeye aliyechukua silaha zake hawapo. 18 Basi Sauli akamwambia Ahiya, Lilete hapa sanduku la Mungu. Kwa kuwa hilo sanduku la Mungu wakati huo lilikuwapo pamoja na wana wa Israeli 19 Ikawa Sauli alipokuwa katika kusema na kuhani, hayo makelele katika marago ya Wafilisti yakaendelea na kuzidi; basi Sauli akamwambia kuhani, Rudisha mkono wako. 20 Naye Sauli na watu wote waliokuwapo pamoja naye wakakusanyika, wakaenda vitani; na tazama, huko upanga wa kila mtu ulikuwa juu ya mwenziwe, kukawa fujo tele kabisa. 21 Basi na wale Waebrania waliokuwa pamoja na Wafilisti tangu zamani, wale waliopanda pamoja nao mpaka maragoni toka nchi iliyozunguka; watu hao nao wakageuka kuwa upande wa Waisraeli waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani. 22 Na vile vile watu wote wa Israeli waliokuwa wamejificha katika nchi ya milima milima ya Efraimu, waliposikia ya kwamba Wafilisti wamekimbia, hata hao nao wakawafuatia mbio vitani. 23 Hivyo Bwana akawaokoa Israeli siku ile; na vita vikapita mbele karibu na Beth-aveni. Wakati huo mbele ya wana wa Israeli. 24 Nao watu wa Israeli walisumbuka sana siku ile; lakini Sauli alikuwa amewaapisha watu, akisema, Na alaaniwe mtu awaye yote alaye chakula cho chote hata jioni, nipate kujilipiza kisasi juu ya adui zangu. Basi hakuna mtu miongoni mwa watu aliyeonja chakula. 25 Nao watu wote wakaingia mwituni; na humo mlikuwa na asali juu ya nchi. 26 Na hapo watu walipokwisha kuingia mwituni, tazama, hiyo asali ilikuwa ikidondoka; walakini hakuna mtu hata mmoja aliyetia mkono wake kinywani; kwa sababu hao watu walikuwa wakikiogopa kile kiapo. 27 Ila Yonathani hakusikia, hapo babaye alipowaagiza watu kwa kiapo; basi yeye akainyosha ncha ya fimbo iliyokuwa mkononi mwake, na kuichovya katika sega la asali, kisha akatia mkono wake kinywani; na macho yake yakatiwa nuru. 28 Ndipo mmojawapo wa watu akamjibu, akasema, Baba yako aliwaagiza watu sana kwa kiapo, akisema, Na alaaniwe mtu alaye chakula leo. Na hao watu walikuwa wamepungukiwa na nguvu. 29 Ndipo Yonathani akasema, Babangu ameifadhaisha nchi; tafadhali, angalia jinsi macho yangu yalivyotiwa nuru, kwa sababu nalionja asali hii kidogo. 30 Je! Si zaidi sana, kama watu wangalikula na kushiba leo katika nyara hizi za adui zao walizoziteka? Kwa maana haukuwa uuaji mkuu sasa katikati ya Wafilisti. 31 Nao wakawapiga watu miongoni mwa Wafilisti siku ile kutoka Mikmashi mpaka Ayaloni; na hao watu walikuwa wamepungukiwa sana na nguvu. 32 Basi watu wakazirukia zile nyara, wakatwaa kondoo, na ng'ombe, na ndama, na kuwachinja papo hapo juu ya nchi, nao wale watu walikuwa wakiwala pamoja na damu. 33 Ndipo wakamwambia Sauli, wakisema, Angalia, watu hao wanakosa juu ya Bwana, kwa jinsi wanavyokula pamoja na damu. Naye akasema, Ninyi mmefanya kwa hiana; vingirisheni kwangu leo jiwe kubwa. 34 Kisha Sauli akasema, Haya! Tawanyikeni katikati ya watu mkawaambie, Nileteeni hapa kila mtu ng'ombe wake, na kila mtu kondoo wake, mkawachinje hapa na kula; wala msikose juu ya Bwana, kwa kula pamoja na damu. Nao watu wote wakaleta kila mtu ng'ombe wake pamoja naye usiku ule, nao wakawachinja hapo. 35 Naye Sauli akamjengea Bwana madhabahu; hiyo ndiyo madhabahu ya kwanza aliyomjengea Bwana. 36 Kisha Sauli akasema, Haya! Na tushuke kuwafuata Wafilisti wakati wa usiku, na kuwateka nyara hata mapambazuko, wala tusiwaache hata mmoja wao. Nao wakamjibu, Fanya yo yote uyaonayo kuwa ni mema. Ndipo yule kuhani akasema, Na tumkaribie Mungu hapa. 37 Basi Sauli akataka shauri kwa Mungu, Je! Nishuke ili kuwafuatia Wafilisti? Je! Utawatia mikononi mwa Israeli? Lakini hakumjibu neno lo lote siku ile. 38 Ndipo Sauli akasema, Karibieni hapa, enyi wakuu wote wa watu; mjue na kuona dhambi hii ya leo imekuwa katika kosa gani. 39 Kwa maana, aishivyo Bwana, awaokoaye Israeli, ijapokuwa i katika Yonathani, mwanangu, kufa atakufa. Lakini miongoni mwa watu wote hakuna mtu ye yote aliyemjibu. 40 Ndipo akawaambia Israeli wote, Ninyi mtakuwa upande mmoja, na mimi na mwanangu Yonathani tutakuwa upande wa pili. Basi wakamwambia Sauli, Fanya uonayo kuwa ni mema. 41 Kwa hiyo Sauli akamwambia Bwana, Mungu wa Israeli, [Kwani usimjibu mtumishi wako leo? Ikiwa dhambi i ndani yangu, au ndani yake Yonathani mwanangu, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, utoe Urimu; bali ukisema hivi, Dhambi i katika watu wako Israeli,] utoe Thumimu ,Basi Yonathani na Sauli wakatwaliwa,lakini watu wakapona. 42 Basi Sauli akasema, Sasa piga kati ya mimi na mwanangu Yonathani, [naye awaye yote ambaye Bwana atamtwaa, atakufa. Nao watu wakamwambia Sauli, La! Sivyo hivyo; lakini Sauli akawaweza watu. Nao wakapiga kati ya yeye na mwanawe Yonathani,] 43 Ndipo Sauli akamwambia Yonathani, Niambie ulilolifanya. Basi Yonathani akamwambia, akasema, Ni kweli, mimi nalionja asali kidogo kwa ncha ya fimbo ile iliyokuwa mkononi mwangu; na tazama, imenipasa kufa. 44 Naye Sauli akasema, Mungu anifanyie hivi, na kuzidi; kwa kuwa hakika utakufa, Yonathani. 45 Walakini watu wakamwambia Sauli, Je! Atakufa Yonathani, ambaye ndiye aliyeufanya huo wokovu mkuu katika Israeli? Hasha! Aishivyo Bwana, hautaanguka chini hata unywele mmoja wa kichwa chake; kwa maana ametenda kazi pamoja na Mungu leo. Hivyo hao watu wakamponya Yonathani, asife. 46 Ndipo Sauli akakwea kuacha kuwafuata Wafilisti; nao Wafilisti wakaenda zao kwao. 47 Basi Sauli alipokwisha kuutwaa ufalme juu ya Israeli, alipigana na adui zake zote pande zote, juu ya Moabu, na juu ya wana wa Amoni, na juu ya Edomu, na juu ya wafalme wa Soba, na juu ya Wafilisti; na po pote alipogeukia, akawashinda. 48 Naye akatenda kwa ushujaa, akawapiga Waamaleki, na kuwaokoa Waisraeli katika mikono yao waliowateka nyara. 49 Basi, wana wa Sauli walikuwa ni hawa, Yonathani, na Ishvi, na Malkishua; na majina ya binti zake wawili yalikuwa haya; jina lake wa kwanza aliitwa Merabu, na jina lake mdogo aliitwa Mikali; 50 na jina lake mkewe Sauli aliitwa Ahinoamu, binti Ahimaasi. Tena, jina la jemadari wa jeshi lake aliitwa Abneri, mwana wa Neri, aliyekuwa baba mdogo wa Sauli. 51 Na Kishi, babaye Sauli, na Neri, babaye Abneri, walikuwa wana wa Abieli. 52 Tena, kulikuwa na vita vikali sana juu ya Wafilisti siku zote za Sauli, naye Sauli alipomwona mtu ye yote aliyekuwa hodari, au mtu ye yote aliyekuwa shujaa, humtwaa ili awe pamoja naye.

1 Samweli 15

1 Wakati huo Samweli akamwambia Sauli, Bwana alinipeleka nikutie mafuta, uwe mfalme wa watu wake Israeli; basi sasa, isikilize sauti na maneno ya Bwana. 2 Bwana wa majeshi asema hivi, Nimeyatia moyoni mwangu mambo hayo Amaleki waliyowatenda Israeli, jinsi walivyowapinga njiani, hapo walipopanda kutoka Misri. 3 Basi sasa enda ukawapige Amaleki, na kuviharibu kabisa vitu vyote walivyo navyo, wala msiwaachilie; bali waueni, mwanamume na mwanamke, mtoto naye anyonyaye, ng'ombe na kondoo, ngamia na punda. 4 Ndipo Sauli akawaita watu, akawahesabu huko Telemu, askari waliopanda farasi mia mbili elfu, na watu wa Yuda kumi elfu. 5 Sauli akaufikilia mji wa Amaleki, akauvizia bondeni. 6 Sauli akawaambia Wakeni, Haya! Enendeni zenu, mkashuke ili kujitenga na Waamaleki, nisije nikawaangamiza ninyi pamoja nao; maana mliwatendea wana wa Israeli mema, walipopanda kutoka Misri. Basi hao Wakeni wakaondoka, wakajitenga na Waamaleki. 7 Sauli akawapiga Waamaleki, toka Havila uendapo Shuri, unaokabili Misri. 8 Akamkamata Agagi, mfalme wa Waamaleki, yu hai, akawaangamiza hao watu wote kwa upanga. 9 Lakini Sauli na watu wake wakamwacha Agagi hai, na katika kondoo walio wazuri, na ng'ombe, na vinono, na wana-kondoo, na cho chote kilicho chema, wala hawakukubali kuwaangamiza; bali cho chote kilichokuwa kibaya na kibovu, ndicho walichokiangamiza kabisa. 10 Ndipo neno la Bwana likamjia Samweli, kusema, 11 Najuta kwa sababu nimemtawaza Sauli awe mfalme; maana amerudi nyuma, asinifuate, wala hakufanya nilivyomwamuru. Samweli akasikitika, akamlilia Bwana usiku kucha. 12 Samweli akaondoka asubuhi na mapema ili aonane na Sauli; Samweli akaambiwa ya kwamba, Sauli alifika Karmeli, na tazama, akajisimamishia ukumbusho, akageuka, akapita, akatelemkia Gilgali. 13 Samweli akamwendea Sauli; naye Sauli akamwambia, Ubarikiwe na Bwana, nimeitimiza amri ya Bwana. 14 Samweli akasema, Maana yake nini, basi, hiki kilio cha kondoo masikioni mwangu, na huu mlio wa ng'ombe ninaousikia? 15 Sauli akasema, Wamewaleta kutoka kwa Waamaleki; maana watu waliwaacha hai kondoo na ng'ombe walio wazuri, ili wawatoe dhabihu kwa Bwana, Mungu wako, nao waliosalia tumewaangamiza kabisa. 16 Ndipo Samweli akamwambia Sauli, Ngoja, nami nitakuambia neno aliloniambia Bwana usiku huu. Naye akamwambia, Haya, sema. 17 Basi Samweli akasema, Ingawa ulikuwa mdogo machoni pako mwenyewe, je! Hukufanywa kuwa kichwa cha kabila za Israeli? Naye Bwana akakutia mafuta uwe mfalme wa Israeli. 18 Kisha Bwana akakutuma safarini, akasema, Enenda ukawaangamize kabisa wale Waamaleki wenye dhambi, upigane nao hata watakapoangamia. 19 Mbona, basi, hukuitii sauti ya Bwana, bali ukazirukia nyara ukafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana? 20 Sauli akamwambia Samweli, Hakika mimi nimeitii sauti ya Bwana, nami nimemleta Agagi, mfalme wa Waamaleki, tena nimewaangamiza Waamaleki kabisa. 21 Ila watu waliteka nyara, kondoo na ng'ombe walio wazuri, katika vitu vilivyowekwa wakfu, kusudi wavitoe dhabihu kwa Bwana, Mungu wako, huko Gilgali. 22 Naye Samweli akasema, je! Bwana huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu. 23 Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi ni kama ukafiri na vinyago; Kwa kuwa umelikataa neno la Bwana, Yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme. 24 Ndipo Sauli akamwambia Samweli, Nimefanya dhambi; maana nimeihalifu amri ya Bwana, pia na maneno yako; kwa sababu naliwaogopa wale watu, nikaitii sauti yao. 25 Basi sasa, nakuomba, unisamehe dhambi yangu; rudi pamoja nami, nipate kumwabudu Bwana. 26 Samweli akasema, Sitarudi pamoja nawe; kwa sababu umelikataa neno la Bwana, Bwana naye amekukataa wewe, usiwe mfalme wa Israeli. 27 Naye Samweli alipogeuka, aende zake, Sauli akaushika upindo wa vazi lake, nalo likararuka. 28 Basi Samweli akamwambia, Leo Bwana amekurarulia ufalme wa Israeli, naye amempa jirani yako, aliye mwema kuliko wewe. 29 Tena Yeye aliye Nguvu za Israeli hatanena uongo, wala hataona majuto; maana siye mwanadamu, hata ajute. 30 Akasema, Nimekosa; lakini uniheshimu sasa, nakuomba, mbele ya wazee wa watu wangu, na mbele ya Israeli, rudi pamoja nami, nimwabudu Bwana, Mungu wako. 31 Basi Samweli akarudi na kuandamana na Sauli; naye Sauli akamwabudu Bwana. 32 Ndipo Samweli akasema, Nileteeni hapa Agagi, mfalme wa Waamaleki. Basi Agagi akamwendea kwa utepetevu. Naye Agagi akasema, Bila shaka uchungu wa mauti umeondoka. 33 Lakini Samweli akamjibu, Kama upanga wako ulivyofanya wanawake kufiwa na watoto wao, vivyo hivyo mama yako atafiwa miongoni mwa wanawake. Basi Samweli akamkata Agagi vipande mbele za Bwana huko Gilgali. 34 Na baada ya hayo Samweli akaenda zake kule Rama; naye Sauli akakwea kwenda nyumbani kwake huko Gibea ya Sauli. 35 Wala Samweli hakuenda tena kuonana na Sauli hata siku ya kufa kwake; lakini Samweli alikuwa akimlilia Sauli; naye Bwana akaghairi ya kuwa amemtawaza Sauli awe mfalme juu ya Israeli.

1 Samweli 16

1 Bwana akamwambia Samweli, Hata lini utamlilia Sauli, ikiwa mimi nimemkataa asiwamiliki Israeli? Ijaze pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe. 2 Samweli akasema, Nawezaje kwenda? Sauli akipata habari, ataniua. Basi Bwana akasema, Chukua ndama pamoja nawe, ukaseme, Nimekuja ili kumtolea Bwana dhabihu. 3 Ukamwite Yese aje kwenye dhabihu, nami nitakuonyesha utakayotenda; nawe utamtia mafuta yule nitakayemtaja kwako. 4 Samweli akafanya hayo aliyosema Bwana, akaenda Bethlehemu. Wakaja wazee wa mji kumlaki, wakitetemeka, nao wakasema, Je! Umekuja kwa amani? 5 Naye akasema, Naam, kwa amani; nimekuja kumtolea Bwana dhabihu; jitakaseni; njoni pamoja nami kwenye dhabihu. Akawatakasa Yese na wanawe, akawaita kwenye dhabihu. 6 Ikawa walipokuja, alimtazama Eliabu, akasema, Yakini masihi wa BWANA yupo hapa mbele zake. 7 Lakini Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo. 8 Ndipo Yese akamwita Abinadabu, akampitisha mbele ya Samweli. Naye akasema, Bwana hakumchagua huyu. 9 Ndipo Yese akampitisha Shama. Naye akasema, wala Bwana hakumchagua huyu. 10 Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samweli. Samweli akamwambia Yese, Bwana hakuwachagua hawa. 11 Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. 12 Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye. 13 Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama. 14 Basi, roho ya Bwana ilikuwa imemwacha Sauli, na roho mbaya kutoka kwa Bwana ikamsumbua. 15 Nao watumishi wa Sauli wakamwambia, Angalia, sasa roho mbaya kutoka kwa Mungu inakusumbua. 16 Basi bwana wetu na atuamuru sisi watumishi wake waliopo hapa mbele yako watafute mtu aliye stadi wa kupiga kinubi; basi itakuwa, roho ile mbaya kutoka kwa Mungu itakapokujilia, yeye atapiga kinubi kwa mkono wake, nawe utapona. 17 Basi Sauli akawaambia, Vema, nitafutieni mtu aliye stadi wa kupiga kinubi, mkaniletee. 18 Ndipo akajibu mmoja wa watumishi wake akasema, Tazama, nimemwona mwana mmoja wa Yese, Mbethlehemi, aliye stadi wa kupiga kinubi, tena ni mtu shujaa, hodari wa vita, anenaye kwa busara, mtu mzuri, ambaye Bwana yu pamoja naye. 19 Basi Sauli akampelekea Yese wajumbe, akasema, Nipelekee Daudi mwanao, aliye pamoja na kondoo. 20 Yese akatwaa punda, wa kuchukua mikate, na kiriba cha divai, na mwana-mbuzi, akampelekea Sauli kwa mkono wa Daudi mwanawe. 21 Basi Daudi akamwendea Sauli, akasimama mbele yake, naye akampenda sana; naye akapata kuwa mtu wa kumchukulia silaha zake. 22 Kisha Sauli akapeleka watu kwa Yese, akasema, Tafadhali, mwache Daudi asimame mbele yangu; maana ameona kibali machoni pangu. 23 Ikawa, ile roho mbaya kutoka kwa Mungu ilipomjilia Sauli, ndipo Daudi akakishika kinubi, akakipiga kwa mkono wake, naye Sauli akaburudishwa, na ile roho mbaya ikamwacha.

1 Samweli 17

1 Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. 2 Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti. 3 Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. 4 Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. 5 Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. 6 Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. 7 Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. 8 Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. 9 Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. 10 Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. 11 Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana. 12 Basi Daudi alikuwa mwana wa yule Mwefrathi, wa Bethlehemu ya Yuda, aliyeitwa jina lake Yese; naye huyo alikuwa na wana wanane; na yeye mwenyewe alikuwa mzee siku za Sauli, na mkongwe miongoni mwa watu. 13 Nao wale wana watatu wa Yese waliokuwa wakubwa walikuwa wamefuatana na Sauli kwenda vitani, na majina ya hao wanawe watatu waliokwenda vitani ni haya, mzaliwa wa kwanza Eliabu, na wa pili wake Abinadabu, na wa tatu Shama. 14 Naye huyo Daudi alikuwa mdogo wa wote; na hao watatu waliokuwa wakubwa wakafuatana na Sauli. 15 Basi Daudi alikuwa akienda kwa Sauli na kurudi ili awalishe kondoo za baba yake huko Bethlehemu. 16 Naye yule Mfilisti hukaribia asubuhi na jioni, akajitokeza siku arobaini. 17 Ndipo Yese akamwambia Daudi mwanawe, Haya! Sasa uwachukulie ndugu zako efa ya bisi, na mikate hii kumi, ipeleke upesi kambini kwa ndugu zako; 18 ukampelekee akida wa elfu yao jibini hizi kumi, ukawaangalie, wa hali gani, kisha uniletee jawabu yao. 19 Basi Sauli, na watu wote wa Israeli, walikuwa katika bonde la Ela, wakipigana na Wafilisti. 20 Daudi akaondoka asubuhi na mapema, akawaacha kondoo pamoja na mchungaji, akavitwaa vitu vile, akaenda, kama Yese alivyomwamuru; akafika penye magari, wakati lile jeshi walipokuwa wakitoka kwenda kupigana, wakipiga kelele za vita. 21 Nao Waisraeli na Wafilisti wakajipanga, jeshi hili likikabili jeshi hili. 22 Basi Daudi akaviacha vile vyombo vyake katika mkono wa mlinda vyombo, akalikimbilia jeshi, akafika, akawasalimu ndugu zake. 23 Hata alipokuwa akisema nao, kumbe! Yule shujaa alitokea, yule Mfilisti wa Gathi, jina lake Goliathi, akitoka katika jeshi la Wafilisti, akasema maneno yale yale; naye Daudi akayasikia. 24 Na watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana. 25 Watu wa Israeli wakasema, Je! Mmemwona mtu huyu aliyepanda huko? Hakika ametokea ili awatukane Israeli; basi, itakuwa, mtu yule atakayemwua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israeli. 26 Daudi akaongea na watu waliosimama karibu, akisema, Je! Atafanyiwaje yeye atakayemwua Mfilisti huyo, na kuwaondolea Israeli aibu hii? Maana Mfilisti huyu asiyetahiriwa ni nani hata awatukane majeshi ya Mungu aliye hai? 27 Nao watu wakamjibu vivyo hivyo, wakisema, Ndivyo atakavyofanyiwa mtu yule atakayemwua. 28 Naye Eliabu, mkubwa wake, alisikia hapo alipoongea na watu; na hasira yake Eliabu ikawaka juu ya Daudi, akasema, Mbona wewe umeshuka hapa? Na kondoo wale wachache umemwachia nani kule nyikani? Mimi nakujua kiburi chako, na ubaya wa moyo wako; maana umeshuka ili upate kuvitazama vita. 29 Naye Daudi akamjibu, Je! Mimi nimekosa nini sasa? Je! Si neno kubwa hilo? 30 Naye akamgeukia ili kumwelekea mtu mwingine, akasema naye jinsi ile ile; na watu wakamjibu tena jinsi ile ile kama ya kwanza. 31 Na maneno hayo aliyosema Daudi yaliposikiwa, watu wakamweleza Sauli; naye akatuma mtu kwenda kumwita. 32 Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. 33 Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake. 34 Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, 35 mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. 36 Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. 37 Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe. 38 Ndipo Sauli akamvika Daudi mavazi yake ya vita, akamtia chapeo cha shaba kichwani, akamvika dirii. 39 Naye Daudi akajifunga upanga juu ya mavazi yake, akajaribu kwenda; maana alikuwa hajavijaribu. Daudi akamwambia Sauli, Siwezi kwenda na vitu hivi, maana sikuvijaribu. Basi Daudi akavivua. 40 Akaichukua fimbo yake mkononi, akajichagulia mawe laini matano katika kijito cha maji, akayatia katika mfuko wa kichungaji aliokuwa nao, maana ni mkoba wake, na kombeo lake alikuwa nalo mkononi mwake, akamkaribia yule Mfilisti. 41 Huyo Mfilisti naye akamsogelea Daudi na kumkaribia; na mtu yule aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. 42 Hata Mfilisti alipotazama huku na huku, akamwona Daudi akamdharau; kwa kuwa ni kijana tu mwekundu, tena ana sura nzuri. 43 Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake. 44 Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni. 45 Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. 46 Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. 47 Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu. 48 Ikawa, hapo Mfilisti alipojiinua, akaenda akamkaribia Daudi, ndipo Daudi naye akapiga mbio, akalikimbilia jeshi ili akutane na yule Mfilisti. 49 Daudi akatia mkono wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga Mfilisti katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka chini kifudifudi. 50 Hivyo Daudi akamshinda yule Mfilisti kwa kombeo na jiwe, akampiga Mfilisti, akamwua; walakini Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake. 51 Ndipo Daudi akapiga mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake, akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa wao amekufa, wakakimbia. 52 Nao watu wa Israeli na wa Yuda wakainuka, na kupiga kelele, nao wakawafuata Wafilisti mpaka ufikapo Gathi, na mpaka malango ya Ekroni. Nao majeruhi wa Wafilisti wakaanguka kando ya njia iendayo Shaarimu, mpaka Gathi, na mpaka Ekroni. 53 Kisha wana wa Israeli wakarudi kutoka katika kuwafukuza Wafilisti, wakateka nyara marago yao. 54 Naye Daudi akakitwaa kichwa chake yule Mfilisti na kukileta Yerusalemu; lakini silaha zake akaziweka hemani mwake. 55 Basi Sauli, hapo alipomwona Daudi akitoka ili kumwendea yule Mfilisti, alimwambia Abneri, jemadari wa jeshi, Je! Abneri, kijana huyu ni mwana wa nani? Abneri akamjibu, Ee mfalme, kama iishivyo roho yako, mimi siwezi kusema. 56 Basi mfalme akasema, Uliza wewe, kijana huyu ni mwana wa nani. 57 Hata na Daudi alipokuwa yuarudi kutoka katika kumwua yule Mfilisti, Abneri alimtwaa, akamleta mbele ya Sauli, naye anacho kichwa chake yule Mfilisti mkononi mwake. 58 Basi Sauli akamwuliza, Wewe, kijana, u mwana wa nani? Naye Daudi akamjibu, Mimi ni mwana wa mtumishi wako, Yese, mtu wa Bethlehemu.

1 Samweli 18

1 Ikawa Daudi alipokwisha kusema na Sauli, roho ya Yonathani, ikaambatana na roho ya Daudi, Yonathani akampenda kama roho yake mwenyewe. 2 Sauli akamtwaa siku ile, wala hakumwacha arudi tena nyumbani kwa baba yake. 3 Nao Yonathani na Daudi wakaahidiana, kwa kuwa alimpenda kama roho yake mwenyewe. 4 Ndipo Yonathani akalivua joho alilokuwa amelivaa, akampa Daudi, na mavazi yake, hata na upanga wake pia, na upinde wake, na mshipi wake. 5 Basi Daudi akatoka kwenda kila mahali alikotumwa na Sauli, akatenda kwa akili; Sauli akamweka juu ya watu wa vita; jambo hili likawa jema machoni pa watu wote, na machoni pa watumishi wa Sauli pia. 6 Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. 7 Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. 8 Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme? 9 Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile. 10 Ikawa siku ya pili yake, roho mbaya kutoka kwa Mungu ikamjilia Sauli kwa nguvu, naye akatabiri ndani ya nyumba. Basi Daudi alikuwa akipiga kinubi kwa mkono wake kama siku zote; naye Sauli alikuwa na mkuki mkononi mwake. 11 Mara Sauli akautupa ule mkuki; maana alisema, Nitampiga Daudi hata ukutani. Daudi akaepa, akatoka mbele yake, mara mbili. 12 Sauli akamwogopa Daudi, kwa sababu Bwana alikuwa pamoja naye, ila amemwacha Sauli. 13 Kwa ajili ya hayo Sauli akamwondosha kwake, akamfanya awe akida wake juu ya askari elfu; naye akatoka na kuingia mbele ya watu. 14 Naye Daudi akatenda kwa busara katika njia zake zote naye Bwana alikuwa pamoja naye. 15 Sauli alipoona ya kwamba alitenda kwa busara sana, yeye alimwogopa. 16 Lakini Israeli wote na Yuda wakampenda Daudi; kwa kuwa alitoka na kuingia mbele yao. 17 Kisha Sauli akamwambia Daudi, Tazama, binti yangu mkubwa, Merabu, huyu nitakupa wewe ili umwoe; ila na wewe uniwie hodari wa vita, na kuvipiga vita vya Bwana. Maana Sauli alisema moyoni mwake, Mkono wangu usiwe juu yake, bali mkono wa Wafilisti na uwe juu yake. 18 Naye Daudi akamwambia Sauli, Mimi ni nani, na jamaa zangu ni akina nani, au mbari ya babangu, katika Israeli, hata mimi niwe mkwewe mfalme? 19 Lakini ikawa, wakati ule, ilipopasa Daudi apewe Merabu, binti Sauli, aliolewa na Adrieli, Mmeholathi. 20 Walakini Mikali, binti Sauli, alimpenda Daudi; watu wakamwambia Sauli, na neno hilo likampendeza. 21 Naye Sauli akasema moyoni, Mimi nitamwoza huyu, awe mtego kwake, tena kwamba mkono wa Wafilisti uwe juu yake. Basi Sauli akamwambia Daudi mara ya pili, Leo utakuwa mkwe wangu. 22 Naye Sauli akawaagiza watumishi wake, Zungumzeni na Daudi kwa siri, na kusema, Angalia, mfalme anakuridhia, na watumishi wake wote wanakupenda; haya basi! Na uwe mkwewe mfalme. 23 Nao watumishi wa Sauli wakanena maneno hayo masikioni mwa Daudi. Daudi akasema, Je! Ninyi mwaona kuwa ni shani mimi kuwa mkwewe mfalme, nami ni maskini, tena sina cheo? 24 Na hao watumishi wa Sauli wakampasha habari, wakisema, Ndivyo hivyo alivyosema Daudi. 25 Naye Sauli akasema, Mwambieni Daudi hivi, Mfalme hataki mahari yo yote, ila anataka govi mia za Wafilisti, ili ajilipize kisasi adui za mfalme. Basi Sauli alidhani kumwangamiza Daudi kwa mkono wa Wafilisti. 26 Na watumishi wake walipomwambia Daudi; maneno hayo, ilimpendeza Daudi sana kuwa mkwewe mfalme. Na siku zilikuwa hazijaisha bado; 27 basi Daudi akainuka, akaenda yeye na watu wake, akaua katika Wafilisti watu mia mbili; na Daudi akazileta govi zao, wakampa mfalme hesabu kamili, ili awe mkwewe mfalme. Naye Sauli akamwoza Mikali, binti yake. 28 Sauli akaona na kutambua ya kwamba Bwana alikuwa pamoja na Daudi; na huyo Mikali, binti Sauli, akampenda. 29 Naye Sauli akazidi kumwogopa Daudi; Sauli akawa adui yake Daudi sikuzote. 30 Wakati huo wakuu wa Wafilisti wakatoka; kisha ikawa, kila mara walipotoka, Daudi akatenda kwa busara zaidi ya watumishi wote wa Sauli hivyo jina lake likawa na sifa kuu.

1 Samweli 19

1 Kisha Sauli akasema na mwanawe Yonathani, tena na watumishi wake wote, kwamba wamwue Daudi. 2 Lakini huyo Yonathani, mwana wake Sauli, alikuwa akipendezwa sana na Daudi. Basi Yonathani akamwambia Daudi, akasema, Sauli, baba yangu, anatafuta kukuua; basi, nakusihi, ujiangalie sana asubuhi, ukae mahali pa siri na kujificha; 3 na mimi nitatoka nje na kusimama kando ya babangu huko shambani ulipo wewe, nami nitazungumza na babangu habari zako; nami nikiona neno lo lote nitakuambia. 4 Naye Yonathani akamsifu Daudi kwa Sauli, babaye akamwambia, Mfalme asikose juu ya mtumishi wake, yaani, juu ya Daudi kwa maana yeye hakukosa juu yako, tena matendo yake kwako yamekuwa mema sana. 5 Kwa kuwa alitia uhai wake mkononi mwake, na kumpiga yule Mfilisti, naye Bwana akawatendea Israeli wote wokovu mkuu. Wewe mwenyewe uliona jambo hilo, ukafurahi; basi kwa nini kukosa juu ya damu isiyo na hatia, umwue huyo Daudi bure? 6 Sauli akaisikiliza sauti ya Yonathani; naye Sauli akaapa, Aishivyo Bwana, yeye hatauawa. 7 Basi Yonathani akamwita Daudi, naye Yonathani akamjulisha mambo hayo yote. Kisha Yonathani akamleta Daudi kwa Sauli, naye alikuwa akihudhuria mbele yake, kama kwanza. 8 Baada ya hayo kulikuwa na vita tena; naye Daudi akatoka, naye akapigana na Wafilisti, naye akawaua kwa uuaji mkuu; nao wakakimbia mbele yake. 9 Tena ikawa, roho mbaya kutoka kwa Bwana ilimjilia Sauli, hapo alipoketi ndani ya nyumba yake, akiwa na mkuki wake mkononi mwake; naye Daudi alikuwa akipiga kinubi kwa mkono wake. 10 Sauli akajaribu kumpiga Daudi hata ukutani kwa mkuki wake, ila yeye akaponyoka kutoka mbele ya Sauli, nao huo mkuki akaupiga ukutani; naye Daudi akakimbia, akaokoka usiku ule. 11 Kisha Sauli akatuma wajumbe mpaka nyumbani kwa Daudi, ili wamvizie na kumwua asubuhi; naye Mikali, mkewe Daudi, akamwambia, akasema, Wewe usipojiponya nafsi yako usiku huu, kesho utauawa. 12 Basi Mikali akamtelemsha Daudi dirishani; naye akaenda akakimbia na kuokoka. 13 Ndipo Mikali akakitwaa kinyago, na kukilaza kitandani, akatia na mto wa singa za mbuzi kichwani pake, na kukifunika kwa nguo. 14 Naye Sauli alipotuma wajumbe ili kumkamata Daudi, yeye alisema, Hawezi. 15 Basi Sauli akawatuma hao wajumbe ili wamtazame Daudi, akisema, Mleteni kwangu juu ya kitanda chake, nipate kumwua. 16 Nao wajumbe walipoingia, kumbe! Kuna kinyago kitandani, na mto wa singa za mbuzi kichwani pake! 17 Sauli akamwambia Mikali, Mbona wewe umenidanganya hivi, na kumwacha adui yangu aende, hata ameniponyoka? Naye Mikali akamjibu Sauli, Yeye aliniambia, Niache niende zangu; kwa nini nikuue? 18 Hivyo Daudi akakimbia, akajiponya, akamwendea Samweli huko Rama, akamwambia hayo yote Sauli aliyomtenda. Kisha yeye na Samweli wakaenda na kukaa katika Nayothi. 19 Naye Sauli akaambiwa, kusema, Angalia, yule Daudi yuko katika Nayothi, huko Rama. 20 Basi Sauli akatuma wajumbe ili kumkamata Daudi; nao hapo walipowaona jamaa ya manabii wakitabiri, na Samweli amesimama kama mkuu wao, roho ya Mungu ikawajilia wajumbe wa Sauli, nao pia wakatabiri. 21 Naye Sauli alipoambiwa, alituma wajumbe wengine, wao nao wakatabiri. Naye Sauli akatuma wajumbe tena mara ya tatu, na wao pia wakatabiri. 22 Kisha yeye mwenyewe akaenda Rama, akafika kunako kile kisima kikubwa kilicho huko Seku; akauliza, akasema, Je! Wako wapi Samweli na Daudi? Na mtu mmoja akajibu, Tazama, wako Nayothi, huko Rama. 23 Basi akaenda Nayothi huko Rama, na roho ya Mungu ikamjilia yeye naye, akaendelea mbele, huku anatabiri, mpaka kufika Nayothi huko Rama. 24 Naye akavua nguo zake, akatabiri mbele ya Samweli, akalala uchi mchana kutwa na usiku kucha siku ile. Kwa hiyo watu husema, Je! Sauli pia yumo miongoni mwa manabii?

1 Samweli 20

1 Kisha Daudi akatoka Nayothi huko Rama, akakimbia, akaenda kwa Yonathani, akasema mbele yake, Nimefanya nini? Uovu wangu ni nini? Dhambi yangu mbele ya baba yako ni nini, hata akaitaka roho yangu? 2 Naye akamwambia, Hasha! Hutakufa; angalia, baba yangu hatendi neno kubwa wala dogo bila kuifunulia mimi, na baba yangu ana sababu gani ya kunificha jambo hili? Sivyo usemavyo. 3 Daudi akaapa, akasema, Baba yako anajua sana ya kuwa nimeona kibali machoni pako, naye asema, Yonathani asilijue neno hili, asije akahuzunika; lakini ni kweli, aishivyo Bwana, na iishivyo roho yako, iko hatua moja tu kati ya mimi na mauti. 4 Ndipo Yonathani akamwambia Daudi, Kadiri roho yako itakavyo, nitakutendea. 5 Naye Daudi akamwambia Yonathani, Tazama, kesho ni mwandamo wa mwezi, nami hainipasi kukosa kuketi chakulani pamoja na mfalme; lakini niache nijifiche bondeni hata siku ya tatu jioni. 6 Baba yako akiona ya kuwa sipo basi sema, Daudi alitaka sana nimpe ruhusa, aende upesi Bethlehemu, mji wake, kwa maana iko huko dhabihu ya mwaka kwa ajili ya jamaa yake yote. 7 Basi, akisema, Ni vema, mimi mtumishi wako nitakuwa na amani; bali akikasirika, ujue ya kuwa amekusudia kutenda jambo baya. 8 Basi, unitendee mema mimi mtumishi wako; kwa sababu umenitia mimi mtumishi wako katika agano la Bwana pamoja nawe, lakini ikiwa mna uovu moyoni mwangu, uniue wewe mwenyewe; kwa nini kunileta kwa baba yako? 9 Naye Yonathani akasema, Haya na yawe mbali nawe, kwa maana kama ningejua ya kuwa baba yangu amekusudia kukutenda neno baya, je! Singekuambia? 10 Basi Daudi akamwambia Yonathani, Ni nani atakayeniambia, ikiwa baba yako amekujibu maneno makali? 11 Yonathani akamwambia Daudi, Twende zetu nje mashambani. Wakatoka wote wawili, wakaenda mashambani. 12 Naye Yonathani akamwambia Daudi, Bwana, Mungu wa Israeli, na awe shahidi; nitakapokuwa nimekwisha kumwuliza baba yangu, kama wakati huu kesho, au siku ya tatu, angalia, kama liko neno jema la kumfaa Daudi, je! Nisikupelekee habari na kukufunulia neno hili? 13 Bwana anitende mimi, Yonathani, hivyo, na kuzidi, ikiwa yampendeza babangu kukutenda mabaya, nisipokufunulia haya, na kukupeleka uende zako kwa amani; na Bwana awe pamoja nawe, kama alivyokuwa pamoja na baba yangu. 14 Nawe utanionyesha fadhili za Bwana, ili nisife, si wakati huu tu maadamu mimi ni hai; 15 lakini pamoja na hayo, hata jamaa yangu pia hutawaondolea kabisa fadhili zako; la, hata wakati ule Bwana atakapokuwa amewaondoa kabisa adui za Daudi wote pia katika uso wa nchi. 16 Basi Yonathani akafanya agano na jamaa yake Daudi, akisema, Bwana naye atayataka mkononi mwa adui zake Daudi. 17 Naye Yonathani akamwapisha Daudi mara ya pili, kwa ajili ya upendo aliokuwa nao kwake; kwa maana alimpenda kama alivyoipenda roho yake mwenyewe. 18 Kisha Yonathani akamwambia, Kesho ni mwandamo wa mwezi, nawe utakosekana, kwa sababu kiti chako kitakuwa hakina mtu. 19 Nawe ukiisha kungoja siku tatu, shuka upesi ufike kuko huko ulikojificha, siku ya shughuli ile; nawe kaa karibu na kile kichuguu kule. 20 Nami nitapiga mishale mitatu kando-kando yake, kana kwamba ninapiga shabaha. 21 Kisha, angalia, nitamtuma mtoto na kumwambia, Nenda ukaitafute mishale. Hapo nikimwambia yule mtoto, Tazama, mishale iko upande wako huu, itwae; basi uje, maana iko amani kwako, wala hapana hatari, Bwana aishivyo. 22 Bali nikimwambia yule mtoto, Tazama, mishale iko huko mbele yako; basi enenda zako, kwa maana Bwana amekuamuru uende zako. 23 Na kwa habari ya neno lile tulilonena, wewe na mimi, angalia Bwana yu kati ya wewe na mimi milele. 24 Basi Daudi akajificha shambani; na mwezi ulipoandama, mfalme aliketi kula chakula. 25 Mfalme aliketi kitini mwake kama sikuzote, katika kiti kilichokuwa karibu na ukuta; Yonathani alikuwa mbele yake; Abneri naye akaketi karibu na Sauli; lakini mahali pake Daudi palikuwa hapana mtu. 26 Lakini Sauli hakusema neno siku ile; maana alidhani ya kuwa, Amepatikana na neno, hakutakata; hakosi yeye hakutakata. 27 Hata siku ya pili baada ya mwandamo wa mwezi, mahali pake palikuwa hapana mtu; basi Sauli akamwambia Yonathani mwanawe, Mbona mwana wa Yese haji kula chakula, jana wala leo? 28 Naye Yonathani akamjibu Sauli, Daudi alitaka sana nimpe ruhusa aende Bethlehemu; 29 akasema, Tafadhali nipe ruhusa niende; kwa maana jamaa yetu wana dhabihu mjini mwetu; na ndugu yangu ameniamuru niende; basi sasa, kama nimeona kibali machoni pako, nakuomba, niondoke; nikawatazame ndugu zangu. Ndiyo sababu hakuja mezani pa mfalme. 30 Basi hasira yake Sauli ikawaka juu ya Yonathani, akamwambia, Wewe, mwana wa mke mkaidi, asi, je! Mimi sijui ya kuwa umemchagua huyo mwana wa Yese, kwa aibu yako mwenyewe, na kwa aibu ya uchi wa mama yako. 31 Maana wakati mwana wa Yese akiwa hai juu ya nchi, wewe hutafanikiwa, wala ufalme wako. Basi, sasa peleka, ukamlete kwangu, maana hakika yake atakufa huyu. 32 Yonathani akamjibu Sauli, baba yake, akamwambia, Auawe kwa sababu gani? Amefanya nini? 33 Sauli akamtupia mkuki wake ili kumpiga; basi Yonathani akajua ya kuwa baba yake ameazimu kumwua Daudi. 34 Basi Yonathani akaondoka pale mezani, mwenye hasira kali, wala hakula chakula siku ya pili ya mwezi, kwa sababu alimhuzunikia Daudi sana, na kwa sababu baba yake amemwaibisha. 35 Hata asubuhi Yonathani akatoka kwenda shambani wakati ule alioagana na Daudi, na mtoto mdogo alikuwa pamoja naye. 36 Akamwambia mtoto wake, Piga mbio, ukaitafute mishale niipigayo. Na yule mtoto alipokuwa akipiga mbio, akapiga mshale, ukapita juu yake. 37 Na mtoto alipofika penye ule mshale alioupiga Yonathani, Yonathani akampigia mtoto kelele, akasema, Je! Mshale si huko mbele yako? 38 Yonathani akampigia mtoto kelele, Haya! Hima! Usikawie. Mtoto wa Yonathani akaikusanya mishale, akaenda kwa bwana wake. 39 Lakini yule mtoto hakujua lo lote. Yonathani na Daudi ndio walioijua habari yenyewe. 40 Naye Yonathani akampa mtoto silaha zake, akamwambia, Nenda, ukazichukue mjini. 41 Basi mara alipokuwa amekwisha ondoka yule mtoto, mara Daudi akatoka mahali pale karibu na kile kichuguu, akaanguka kifudifudi, akajiinama mara tatu; nao wakabusiana, wakaliliana, hata Daudi akazidi. 42 Naye Yonathani akamwambia Daudi, Enenda kwa amani; kwa maana sisi sote wawili tumeapiana kwa jina la Bwana ya kwamba, Bwana atakuwa kati ya mimi na wewe, na kati ya uzao wangu na uzao wako milele. Daudi akaondoka, akaenda zake; Yonathani naye akaenda zake mjini.

1 Samweli 21

1 Basi Daudi akaenda Nobu kwa Ahimeleki, kuhani. Ahimeleki akaenda kumlaki Daudi, akitetemeka, akamwambia, Kwani wewe kuwa peke yako, wala hapana mtu pamoja nawe? 2 Daudi akamwambia Ahimeleki, kuhani, Mfalme ameniagiza shughuli, akaniambia, Asijue mtu awaye yote habari ya shughuli hii ninayokutuma, wala ya neno hili ninalokuamuru; nami nimewaagiza vijana waende mahali fulani. 3 Kuna nini basi, chini ya mkono wako? Nipe mkononi mwangu mikate mitano, au cho chote ulicho nacho hapa. 4 Yule kuhani akamjibu Daudi, akasema, Hapana mikate ya sikuzote chini ya mkono wangu, ila mikate mitakatifu; ikiwa wale vijana wamejitenga na wanawake. 5 Naye Daudi akamjibu kuhani, akamwambia, Hakika tumejitenga na wanawake siku hizi tatu; napo nilipotoka, vyombo vya vijana hawa vilikuwa vitakatifu, ingawa ilikuwa safari ya sikuzote; basi leo je! Vyombo vyetu havitakuwa vitakatifu zaidi? 6 Ndipo kuhani akampa ile mikate mitakatifu; kwa maana hapakuwa na mikate ila ile ya Wonyesho, nayo imekwisha kuondolewa mbele za Bwana, ili itiwe mikate ya moto siku ile ilipoondolewa. 7 Basi siku ile palikuwapo na mtu mmoja wa watumishi wa Sauli, amezuiwa hapo mbele za Bwana jina lake akiitwa Doegi, Mwedomi, mkubwa wa wachungaji wa Sauli. 8 Tena Daudi akamwambia Ahimeleki, Na hapa chini ya mkono wako, je! Hapana mkuki, au upanga? Kwa maana sikuleta upanga, wala silaha zangu, kwa sababu ile shughuli ya mfalme ilitaka haraka. 9 Yule kuhani akasema, upanga wa Goliathi, yule Mfilisti, uliyemwua katika bonde la Ela, tazama, upo hapa, umefungwa ndani ya nguo nyuma ya naivera; ukipenda kuuchukua, haya! Uchukue, maana hapa hapana mwingine ila huo tu. Daudi akasema, Hapana mwingine kama ule; haya! Nipe. 10 Basi Daudi akaondoka, akakimbia siku ile, kwa hofu ya Sauli, akamwendea Akishi, mfalme wa Gathi. 11 Nao watumishi wa Akishi wakamwambia, Je! Huyu siye yule Daudi, mfalme wa nchi? Je! Hawakuimbiana habari zake katika ngoma zao, kusema,Sauli amewaua elfu zake,Na Daudi makumi elfu yake. 12 Naye Daudi akayatia maneno hayo moyoni mwake, akamwogopa sana Akishi, mfalme wa Gathi. 13 Akaubadilisha mwenendo wake mbele yao, akajifanya mwenye wazimu mikononi mwao, akakuna-kuna katika mbao za mlango, na kuyaacha mate yake kuanguka juu ya ndevu zake. 14 Ndipo huyo Akishi akawaambia watumishi wake, Angalieni, mwaona ya kuwa mtu huyu ana wazimu; basi, maana yake nini kumleta kwangu? 15 Je! Mimi nina haja ya watu wenye wazimu, hata mmemleta kiumbe hiki ili aonyeshe wazimu wake machoni pangu? Je! Huyu ataingia nyumbani mwangu?

1 Samweli 22

1 Basi Daudi akaondoka huko, akakimbilia pango la Adulamu; na ndugu zake na watu wote wa mbari ya baba yake waliposikia habari hiyo, wakamwendea huko. 2 Na kila mtu aliyekuwa katika hali ya dhiki, na kila mtu aliyekuwa na deni, na watu wote wenye uchungu mioyoni mwao, wakakusanyika kwake; naye akawa jemadari wao; nao waliokuwa pamoja naye walipata kama watu mia nne. 3 Kutoka huko Daudi akaenda Mispa ya Moabu; akamwambia mfalme wa Moabu, Tafadhali ukubali baba yangu na mama yangu watoke huko waliko, wakakae kwenu, hata nitakapojua Mungu atakalotenda kwa ajili yangu. 4 Akawaleta mbele ya mfalme wa Moabu, nao wakakaa pamoja naye wakati wote Daudi alipokuwa ngomeni. 5 Kisha nabii Gadi akamwambia Daudi, Usikae hapa ngomeni; ondoka, ukaende mpaka nchi ya Yuda. Ndipo Daudi akaondoka, akaenda zake, akakaa katika msitu wa Herethi. 6 Kisha Sauli akasikia ya kwamba Daudi ameonekana, na wale watu waliokuwa pamoja naye. Basi Sauli alikuwa akikaa Gibea, chini ya mkwaju katika mahali palipoinuka, naye alikuwa na mkuki wake mkononi, na watumishi wake wote wakimzunguka. 7 Naye Sauli akawaambia watumishi wake waliomzunguka, Sikieni sasa, enyi Wabenyamini; je! Huyu mwana wa Yese atawapa ninyi kila mmoja mashamba, na mashamba ya mizabibu, atawafanya kuwa maakida wa watu elfu, na maakida wa watu mia; 8 hata ninyi nyote mkafanya fitina juu yangu, wala hapana mtu anifunuliaye habari hii mwanangu afanyapo agano na mwana wa Yese, wala hapana mmoja wenu anayenisikitikia, wala kunifunulia ya kuwa mwanangu amemwondokesha mtumishi wangu juu yangu, anivizie kama hivi leo? 9 Ndipo akajibu Doegi, Mwedomi, aliyesimama karibu na watumishi wa Sauli, akasema, Mimi nalimwona mwana wa Yese akienda Nobu, kwa Ahimeleki, mwana wa Ahitubu. 10 Naye akamwuliza Bwana kwa ajili yake, akampa vyakula, akampa na ule upanga wa Goliathi, Mfilisti. 11 Ndipo mfalme akatuma watu waende kumwita Ahimeleki, kuhani, mwana wa Ahitubu, na jamaa yote ya baba yake, hao makuhani, waliokuwako huko Nobu; nao wakaenda kwa mfalme wote pia. 12 Sauli akasema, Sikia sasa, Ewe mwana wa Ahitubu. Naye akaitika, Mimi hapa, bwana wangu. 13 Sauli akamwuliza, Mbona mmefanya fitina juu yangu, wewe na mwana wa Yese? Kwa maana umempa mikate, na upanga, nawe umemwuliza Mungu kwa ajili yake, ili aniondokee na kunivizia kama hivi leo? 14 Basi Ahimeleki akamjibu mfalme, akasema, Katika watumishi wako wote ni nani aliye mwaminifu kama Daudi, aliye mkwewe mfalme, tena msiri wako, mwenye heshima nyumbani mwako? 15 Je! Mimi nimeanza leo tu kumwuliza Mungu kwa ajili yake? Hasha! Mfalme asinidhanie mimi, mtumishi wake neno hili, Wala jamaa yote ya baba yangu, kwa maana mimi, mtumishi wako siyajui hayo yote, yaliyopungua au yaliyozidi. 16 Naye mfalme akasema, Kufa utakufa, Ahimeleki, wewe na jamaa yote ya baba yako. 17 Kisha mfalme akawaambia askari walinzi waliosimama karibu naye Geukeni, mkawaue hao makuhani wa Bwana, kwa sababu mkono wao u pamoja na Daudi, na kwa sababu walijua ya kuwa amekimbia, wasiniarifu. Lakini watumishi wa mfalme walikataa kunyosha mkono na kuwaangukia makuhani wa Bwana. 18 Basi mfalme akamwambia Doegi, Geuka wewe, ukawaangukia hao makuhani. Basi Doegi, Mwedomi, akageuka, akawaangukia makuhani, akaua siku ile watu themanini na watano wenye kuvaa naivera ya kitani. 19 Kisha akaupiga Nobu, mji wa makuhani, kwa makali ya upanga, wanaume na wanawake, watoto na wanyonyao, na ng'ombe, na punda, na kondoo. 20 Na katika wana wa Ahimeleki, mwana wa Ahitubu, akaokoka mtu mmoja tu, aliyeitwa jina lake Abiathari, akamkimbilia Daudi. 21 Naye Abiathari akamweleza Daudi ya kwamba Sauli amewaua makuhani wa Bwana. 22 Daudi akamwambia Abiathari, Siku ile alipokuwako Doegi, Mwedomi, nalijua yakini ya kuwa atamwambia Sauli; mimi nimewapatia watu wote wa jamaa ya baba yako kifo. 23 Kaa wewe pamoja nami, usiogope; kwa maana yeye atafutaye roho yangu, ndiye atafutaye na roho yako; nawe utakaa kwangu salama.

1 Samweli 23

1 Kisha wakamwambia Daudi, kusema, Angalia, Wafilisti wanapigana vita juu ya Keila na kuiba nafaka sakafuni mwa kupuria. 2 Basi Daudi akamwuliza Bwana, kusema, Je! Niende nikawapige hao Wafilisti? Naye Bwana akamwambia Daudi, Nenda ukawapige Wafilisti, na kuuokoa Keila. 3 Ila watu wake Daudi wakamwambia, Tazama, sisi tunaogopa hapa katika Yuda; je! Si zaidi tukienda Keila juu ya majeshi ya Wafilisti? 4 Basi Daudi akamwuliza Bwana tena, Naye Bwana akamjibu, akasema, Ondoka, ukashukie Keila; kwa kuwa nitawatia hao Wafilisti mikononi mwako. 5 Ndipo wakaenda Keila, Daudi na watu wake, wakapigana na hao Wafilisti, wakateka nyara ng'ombe zao, na kuwaua uuaji mkuu. Hivyo Daudi akawaokoa watu wa Keila. 6 Ikawa Abiathari, mwana wa Ahimeleki, alipomkimbilia Daudi huko Keila, alishuka na naivera mkononi mwake. 7 Kisha Sauli aliambiwa ya kwamba Daudi amefika Keila. Sauli akasema, Mungu amemtia mkononi mwangu; kwa maana amefungwa ndani, kwa vile alivyoingia katika mji wenye malango na makomeo. 8 Basi Sauli akawaita watu wote waende vitani, ili waishukie Keila, na kumhusuru Daudi na watu wake. 9 Naye Daudi alifahamu ya kuwa Sauli amemkusudia mabaya; akamwambia Abiathari, kuhani, Lete hapa hiyo naivera. 10 Ndipo Daudi akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, mimi mtumwa wako nimesikia hakika ya kuwa Sauli anataka kuja huku Keila, ili kuuharibu mji kwa ajili yangu. 11 Je! Watu wa Keila watanitoa, nitiwe mkononi mwake? Je! Sauli atashuka, kama mtumwa wako alivyosikia? Ee Bwana, Mungu wa Israeli, nakusihi, umwambie mtumwa wako. Naye Bwana akamjibu, Atashuka. 12 Ndipo Daudi akasema, Je! Watu wa Keila watanitia mimi na watu wangu mkononi mwake Sauli? Bwana akasema, Watakutia. 13 Basi Daudi na watu wake, ambao wapata kama mia sita, wakaondoka na kutoka Keila, wakaenda po pote walipoweza kwenda. Kisha Sauli akaambiwa ya kwamba Daudi amekimbia toka Keila; akaacha kutoka nje. 14 Basi Daudi alikuwa akikaa nyikani ngomeni, akakaa katika nchi ya milima milima kwenye nyika ya Zifu. Naye Sauli alikuwa akimtafuta kila siku, lakini Mungu hakumtia mikononi mwake. 15 Daudi akaona ya kwamba Sauli ametoka nje ili kutafuta roho yake; naye Daudi akawako katika nyika ya Zifu, huko Horeshi. 16 Ndipo Yonathani, mwana wa Sauli, akainuka akamwendea Daudi huko Horeshi, akamtia nguvu mkono wake katika Mungu. 17 Akamwambia, Usiogope, kwa maana mkono wa Sauli, babangu, hautakupata; na wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli; na mimi nitakuwa wa pili wako; ndivyo ajuavyo hata Sauli, babangu. 18 Na hao wawili wakafanya agano mbele za Bwana; Daudi naye akakaa huko Horeshi, na Yonathani akaenda nyumbani kwake. 19 Ndipo wale Wazifi wakakwea kwa Sauli huko Gibea, wakasema, Je! Yule Daudi hakujificha kwetu ngomeni mwa Horeshi, kilimani pa Hakila upande wa kusini wa Yeshimoni? 20 Basi sasa, Ee mfalme, ushuke, kama utakavyo nafsini mwako kushuka; na kazi yetu itakuwa kumtia mkononi mwa mfalme. 21 Naye Sauli akasema, Na mbarikiwe ninyi na Bwana; kwa sababu mmenihurumia. 22 Nendeni, nawasihi, mkazidi kupata hakika, mkajue na kuona mahali pake anapojificha, tena ni nani aliyemwona huko; maana nimeambiwa ya kwamba atenda kwa hila nyingi. 23 Chunguzeni basi, mkayajue maficho yake yote anapojificha; kisha njoni kwangu, tena msikose, nami nitakwenda pamoja nanyi; tena itakuwa, akiwapo katika nchi, mimi nitamtafuta-tafuta katika elfu zote za Yuda. 24 Nao wakaondoka, wakaenda Zifu kumtangulia Sauli; lakini Daudi na watu wake walikuwapo nyikani pa Maoni, katika Araba upande wa kusini wa jangwa. 25 Basi Sauli na watu wake wakaenda kumtafuta. Watu wakamwambia Daudi; basi kwa hiyo akashuka mpaka mwambani, akakaa nyikani pa Maoni. Naye Sauli alipopata habari, alimwinda Daudi nyikani pa Maoni. 26 Sauli akaenda upande huu wa mlima, na Daudi na watu wake wakaenda upande huu wa mlima; naye Daudi akafanya haraka sana kwenda zake kwa hofu ya Sauli; kwa sababu Sauli na watu wake wakamzunguka Daudi na watu wake ili kuwakamata. 27 Lakini akaja mjumbe kwa Sauli, kusema, Njoo upesi, kwa kuwa Wafilisti wameishambulia nchi. 28 Basi Sauli akarudi kutoka kumwinda Daudi, akaenda kinyume cha Wafilisti; kwa hiyo wakapaita mahali pale, Selahamalekothi. 29 Naye Daudi akakwea kutoka huko, akakaa katika ngome ya Engedi.

1 Samweli 24

1 Ikawa, Sauli aliporudi baada ya kuwafuatia Wafilisti, aliambiwa ya kwamba, Daudi yuko katika nyika ya Engedi. 2 Ndipo Sauli akatwaa watu elfu waliochaguliwa katika Israeli wote, akaenda kumtafuta Daudi na watu wake juu ya majabali ya mbuzi-mwitu. 3 Akafika penye mazizi ya kondoo kando ya njia, na huko kulikuwa na pango; Sauli akaingia ndani ili kuifunika miguu. Na Daudi na watu wake walikuwa wakikaa mle pangoni ndani sana. 4 Nao watu wa Daudi wakamwambia, Tazama, hii ndiyo siku ile aliyokuambia Bwana, Angalia, nitamtia adui yako mikononi mwako, nawe utamtenda yo yote utakayoona kuwa mema. Basi Daudi akainuka, akaukata upindo wa vazi lake Sauli kwa siri. 5 Lakini halafu, moyo wake Daudi ukamchoma, kwa sababu amekata upindo wa vazi lake Sauli. 6 Akawaambia watu wake, Hasha! Nisimtendee bwana wangu, masihi wa BWANA,neon hili,kuunyosha mkono wangu juu yake,kwa maana yeye ni masihi wa BWANA. 7 Basi Daudi akawazuia watu wake kwa maneno hayo, asiwaache kumwondokea Sauli. Kisha Sauli akatoka pangoni, akaenda zake. 8 Daudi naye akainuka baadaye, akatoka pangoni, akamwita Sauli, akisema, Bwana wangu, mfalme. Na Sauli alipotazama nyuma, Daudi akainama uso wake hata nchi, akamsujudia. 9 Daudi akamwambia Sauli, Kwa nini unasikiliza maneno ya watu wasemao, Tazama, Daudi anataka kukudhuru? 10 Tazama, leo hivi macho yako yameona jinsi Bwana alivyokutia mikononi mwangu pangoni, na watu wengine wakaniambia nikuue; lakini nikakuacha; nikasema, Sitaki kuunyosha mkono wangu juu ya bwana wangu; kwa maana yeye ni masihi wa BWANA. 11 Tena, baba yangu, tazama, tafadhali, tazama upindo wa vazi lako mkononi mwangu; maana ikiwa nimeukata upindo wa vazi lako, nisikuue, ujue, na kuona ya kuwa hakuna uovu wala kosa mkononi mwangu, wala sikukukosa neno; ingawa wewe unaniwinda roho yangu ili kuikamata. 12 Bwana atuamue, mimi na wewe, na Bwana anilipizie kisasi changu kwako; lakini mkono wangu hautakuwa juu yako. 13 Kama vile walivyosema watu wa kale katika mithali yao, Katika waovu hutoka uovu; ila mkono wangu hautakuwa juu yako. 14 Na mfalme wa Israeli ametoka ili kumfuatia nani? Unamwinda nani? Ni kuwinda mbwa mfu, au kiroboto. 15 Basi Bwana atuamue, akatuhukumu mimi na wewe, akaone, akanitetee neno langu, akaniokoe na mkono wako. 16 Ikawa, Daudi alipokwisha kumwambia Sauli maneno hayo Sauli alisema, Hii ndiyo sauti yako, Daudi, mwanangu? Naye Sauli akapaza sauti yake, akalia. 17 Akamwambia Daudi, Wewe u mwenye haki kuliko mimi; maana wewe umenitendea mema, nami nimekutenda mabaya. 18 Nawe umeonyesha leo jinsi ulivyonitendea mema, kwani Bwana aliponitia mikononi mwako, hukuniua. 19 Maana mtu akimwona adui yake, je! Atamwacha aende zake salama? Basi Bwana na akulipe mema kwa haya uliyonitendea leo. 20 Na sasa, angalia, najua ya kuwa hakika utakuwa mfalme, na ufalme wa Israeli utafanyika imara mkononi mwako. 21 Basi sasa, uniapie kwa Bwana, ya kwamba hutawakatilia mbali wazao wangu baada yangu, wala hutaliharibu jina langu katika mbari ya baba yangu. 22 Naye Daudi akamwapia Sauli. Kisha Sauli akaenda zake kwao; lakini Daudi na watu wake wakapanda kwenda ngomeni.

1 Samweli 25

1 Akafa Samweli; nao Israeli wote wakakusanyika, wakamwomboleza, wakamzika nyumbani mwake huko Rama. 2 Na huko Maoni kulikuwa na mtu mmoja, ambaye alikuwa na mali yake katika Karmeli; naye yule mtu alikuwa mkuu sana, mwenye kondoo elfu tatu na mbuzi elfu; naye alikuwa akiwakata manyoya kondoo zake huko Karmeli. 3 Na jina la mtu huyo aliitwa Nabali; na jina la mkewe aliitwa Abigaili, na huyo mwanamke alikuwa mwenye akili njema, mzuri wa uso; bali yule mwanamume alikuwa hana adabu, tena mwovu katika matendo yake; naye alikuwa wa mbari ya Kalebu. 4 Basi Daudi akasikia huko nyikani ya kuwa Nabali alikuwa katika kuwakata manyoya kondoo zake. 5 Daudi akatuma vijana kumi, Daudi naye akawaambia hao vijana, Kweeni mwende Karmeli, na kumwendea huyu Nabali ili mnisalimie; 6 na hivi ndivyo mtakavyomwambia huyu aishiye salama, Amani na iwe kwako, na amani nyumbani mwako, na amani kwao wote ulio nao. 7 Nami sasa nimesikia ya kuwa una watu wanaokata manyoya kondoo zako; haya! Wachungaji wako wamekuwa pamoja nasi, wala hatukuwadhuru, wala hawakukosa kitu wakati wote walipokuwako huko Karmeli. 8 Waulize vijana wako, nao watakuambia; basi na wakubaliwe vijana hawa machoni pako; maana tumekujia katika siku ya heri; uwape, nakusihi, cho chote kitakachokujia mkononi, uwape watumwa wako na mwanao Daudi. 9 Basi walipofika vijana wake Daudi, wakamwambia Nabali sawasawa na maneno hayo yote kwa jina la Daudi, kisha wakanyamaza. 10 Naye Nabali akawajibu wale watumishi wa Daudi, akasema, Huyu Daudi ni nani? Na mwana wa Yese ni nani? Siku hizi kuna watumwa wengi wanaomtoroka kila mtu bwana wake! 11 Basi mimi je! Nitwae mkate wangu, na maji yangu, na machinjo yangu niliyowachinjia hao watu wangu wakatao manyoya kondoo zangu, na kuwapa watu ambao siwajui wametoka wapi? 12 Basi vijana wake Daudi wakageuka, wakaenda zao, wakarudi, nao wakaja wakamwambia sawasawa na maneno hayo yote. 13 Kisha Daudi akawaambia watu wake, Haya! Jifungeni kila mtu upanga wake. Nao wakajifunga kila mtu upanga wake; Daudi naye akajifunga upanga wake; nao wakapanda nyuma yake Daudi, wapata kama watu mia nne; na watu mia mbili wakakaa na vyombo vyao. 14 Lakini kijana mmojawapo alimpasha habari Abigaili, mkewe Nabali, kasema, Tazama, Daudi alituma wajumbe kutoka nyikani waje ili kumsalimu bwana wetu, naye akawatukana. 15 Walakini watu hawa walitutendea mema sana, wala hatukupata dhara, wala sisi hatukupotewa na kitu cho chote, wakati wote tulipofuatana nao, tulipokuwako mavueni; 16 watu hao walikuwa boma kwetu usiku na mchana, wakati wote tulipokuwa nao tukiwachunga kondoo. 17 Basi sasa ujue na kufikiri utakayotenda; kwa sababu yamekusudiwa mabaya juu ya bwana wetu, na juu ya nyumba yake yote; kwa kuwa yeye ni mtu asiyefaa kabisa, hata mtu hawezi kusema naye. 18 Ndipo Abigaili akafanya haraka, akatwaa mikate mia mbili, na viriba viwili vya divai, na kondoo watano waliofanyizwa tayari, na vipimo vitano vya bisi, na vishada mia vya zabibu, na mikate ya tini mia mbili; akavipakia vitu hivi juu ya punda. 19 Akawaambia vijana wake, Haya! Tangulieni mbele yangu; angalieni, mimi nawafuata. Ila hakumwambia mumewe, Nabali. 20 Ikawa, alipokuwa amepanda punda wake, na kutelemka penye sitara ya mlima, tazama, Daudi na watu wake walikuwa wakishuka kumkabili; naye akawakuta. 21 Basi Daudi alikuwa amesema, Hakika ni bure nilivyokuwa nikilinda nyikani yote aliyo nayo mtu huyu, asipotewe na kitu cho chote cha mali yake yote; naye amenilipa mabaya badala ya mema. 22 Mungu naye awafanyie hivyo adui za Daudi, na kuzidi, nikimwachia katika wote walio wake hata mtoto mume mmoja, kutakapopambazuka asubuhi. 23 Ndipo hapo Abigaili alipomwona Daudi, alifanya haraka kushuka juu ya punda wake, akamwangukia Daudi kifulifuli, akainama mpaka nchi. 24 Akamwangukia miguuni pake, akasema, Juu yangu, bwana wangu, juu yangu mimi na uwe uovu; tafadhali mjakazi wako na anene masikioni mwako, nawe uyasikilize maneno ya mjakazi wako. 25 Nakusihi, bwana wangu, wewe usimwangalie huyu mtu asiyefaa, yaani, Nabali; kwa maana kama lilivyo jina lake ndivyo alivyo yeye; jina lake ndilo Nabali, na upumbavu anao; lakini mimi, mjakazi wako, sikuwaona hao vijana wa bwana wangu aliowatuma. 26 Basi sasa, bwana wangu, aishivyo Bwana, na iishivyo nafsi yako, kwa kuwa Bwana amekuzuia usimwage damu, tena usijilipize kisasi mkono wako mwenyewe, basi sasa adui zako, na hao wamtakiao bwana wangu mabaya, wawe kama Nabali. 27 Na sasa zawadi hii, mjakazi wako aliyomletea bwana wangu, na wapewe vijana wamfuatao bwana wangu. 28 Nakuomba ulisamehe kosa lake mjakazi wako, kwa kuwa hakika Bwana atamfanyia bwana wangu nyumba iliyo imara, kwa sababu bwana wangu anavipiga vita vya Bwana; tena uovu hautaonekana ndani yako siku zako zote. 29 Na hata ijapokuwa binadamu angeinuka akuwinde, na kuitafuta nafsi yako, hiyo nafsi ya bwana wangu itafungwa katika furushi ya uhai pamoja na Bwana, Mungu wako; na nafsi za adui zako ndizo atakazozitupa nje, kama kutoka kati ya teo. 30 Tena itakuwa, hapo Bwana atakapokuwa amemtendea bwana wangu sawasawa na mema yote aliyoyanena juu yako, na kukutawaza juu ya Israeli; 31 hili halitakuwa kwazo, wala chukizo la moyoni kwa bwana wangu, ama ya kuwa umemwaga damu bure, ama ya kuwa bwana wangu amejilipiza kisasi mwenyewe; tena hapo Bwana atakapokuwa amemtendea bwana wangu mema, ndipo umkumbuke mjakazi wako. 32 Naye Daudi akamwambia Abigaili, Na ahimidiwe Bwana, Mungu wa Israeli, ambaye amekuleta hivi leo kunilaki; 33 na ibarikiwe busara yako, na ubarikiwe wewe, uliyenizuia hivi leo nisimwage damu, wala kujilipiza kisasi kwa mkono wangu mwenyewe. 34 Kwa kuwa ni kweli, aishivyo Bwana, Mungu wa Israeli, aliyenizuia nisikudhuru, kwamba hungefanya haraka kuja kunilaki, hakika huyu Nabali asingaliachiwa hata mtoto mume mmoja, kutakapopambazuka asubuhi. 35 Basi Daudi akapokea mkononi mwake vitu vile alivyomletea; akamwambia, Haya! Kwea kwa amani kwenda nyumbani kwako; tazama, nimeisikiliza sauti yako, nami nimeukubali uso wako. 36 Kisha Abigaili alimjia Nabali; na tazama, alikuwa amefanya karamu nyumbani mwake, kama karamu ya kifalme; na moyo wake huyo Nabali ukafurahiwa ndani yake, kwa maana amelewa kabisa. Kwa sababu hiyo hakumwambia neno, dogo wala kubwa, hata kulipopambazuka. 37 Ikawa asubuhi, divai ilipokuwa imemtoka Nabali, mkewe alimwambia mambo hayo, na moyo wake ukafa ndani yake, akawa kama jiwe. 38 Tena ikawa, yapata siku kumi baadaye, Bwana alimpiga huyo Nabali, hata akafa. 39 Naye aliposikia ya kwamba Nabali amekufa, Daudi alisema, Na ahimidiwe Bwana ambaye amenitetea teto la shutumu langu mkononi mwa Nabali, na kumzuia mtumwa wake asitende maovu; tena uovu wake Nabali Bwana amemrudishia juu ya kichwa chake mwenyewe. Kisha Daudi akatuma watu, akamposa Abigaili ili amwoe. 40 Na hao watumishi wa Daudi walipomjia huyo Abigaili huko Karmeli, walimwambia, wakasema, Daudi ametutuma kwako ili tukutwae uwe mkewe. 41 Naye akainuka na kujiinamisha kifulifuli mpaka nchi, akasema, Tazama, mjakazi wako ni mtumwa wa kuwaosha miguu watumishi wa bwana wangu. 42 Abigaili akafanya haraka, akainuka, akapanda punda, pamoja na vijakazi watano wake waliofuatana naye, akawafuata hao wajumbe wa Daudi, akawa mkewe. 43 Tena Daudi akamwoa Ahinoamu wa Yezreeli; wakawa wote wawili wakeze. 44 Walakini Sauli alikuwa amempa Palti, mwana wa Laishi, aliyekuwa mtu wa Galimu, Mikali binti yake, aliyekuwa mkewe Daudi.

1 Samweli 26

1 Basi hao Wazifi wakamwendea Sauli huko Gibea, wakasema, Je! Yule Daudi hakujificha katika kilima cha Hakila, kuelekea Yeshimoni? 2 Basi Sauli akaondoka, akashuka nyikani kwa Zifu, naye alikuwa na watu elfu tatu, wateule wa Israeli, pamoja naye, ili kumtafuta Daudi katika nyika ya Zifu. 3 Naye Sauli akapiga hema katika kilima cha Hakila, kilichoelekea Yeshimoni, barabarani; lakini Daudi alikuwa akikaa nyikani, akaona ya kwamba Sauli amemfuata mpaka nyikani. 4 Basi Daudi akatuma wapelelezi, akapata habari ya hakika ya kwamba Sauli amefika. 5 Daudi akainuka, akafika mahali pale alipotua Sauli; Daudi akapaangalia mahali alipolala Sauli, na Abneri, mwana wa Neri, jemadari wa jeshi lake; naye Sauli alikuwa amelala kati ya magari, na hao watu wamepiga hema zao wakimzunguka. 6 Ndipo Daudi akajibu, akamwambia Ahimeleki, Mhiti, na Abishai, mwana wa Seruya, ndugu yake Yoabu, akisema, Ni nani atakayeshuka pamoja nami kwa Sauli kambini? Abishai akasema, Mimi nitashuka pamoja nawe. 7 Basi Daudi na Abishai wakawaendea watu usiku; na tazama, Sauli alikuwapo kati ya magari amelala usingizi, na fumo lake limechomekwa chini, karibu na kichwa chake; naye Abneri na watu wake wamelala wakimzunguka. 8 Ndipo Abishai akamwambia Daudi, Mungu amemtia adui yako mikononi mwako leo; basi, niache nimpige kwa hilo fumo hata nchi kwa pigo moja, sitampiga mara ya pili. 9 Lakini Daudi akamwambia Abishai, Usimwangamize; kwani ni nani awezaye kuunyosha mkono wake juu ya masihi 10 Daudi akasema, Aishivyo Bwana, Bwana atampiga; au siku yake ya kufa itampata; atashuka kwenda vitani na kupotea. 11 Hasha! Nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi 12 Basi Daudi akalitwaa lile fumo, na lile gudulia la maji, kichwani pa Sauli; nao wakaenda zao, wala hapana mtu aliyeliona jambo hili wala kulijua, wala kuamka; maana wote walikuwa wamelala; kwa kuwa usingizi mzito kutoka kwa Bwana umewaangukia. 13 Kisha Daudi akaenda ng'ambo ya pili, akasimama juu ya kilima, mbali sana; palipokuwapo nafasi tele katikati yao; 14 naye Daudi akawapigia kelele watu wale, na Abneri, mwana wa Neri, akasema, Abneri, hujibu? Ndipo Abneri akajibu, akasema, U nani wewe unayemlilia mfalme? 15 Naye Daudi akamwambia Abneri, Wewe si mtu shujaa? Tena ni nani aliye sawa na wewe katika Israeli? Mbona, basi, hukumlinda bwana wako, huyo mfalme? Kwa maana mtu mmoja aliingia ili amwangamize mfalme, bwana wako? 16 Jambo hili ulilolitenda si jema. Aishivyo Bwana, mmestahili kufa, kwa sababu hamkumlinda bwana wenu, masihi*fq* wa Bwana. Haya basi! Tazameni, liko wapi fumo la mfalme, na gudulia la maji lililokuwa kichwani pake? 17 Naye Sauli akaitambua sauti ya Daudi, akasema, Hii ndiyo sauti yako, Daudi, mwanangu? Daudi akasema, Ndiyo, ni sauti yangu, bwana wangu, mfalme. 18 Akasema, Bwana wangu ananiwinda mimi mtumishi wake kwa sababu gani? Nimefanya nini mimi? Ni uovu gani nilio nao mkononi mwangu? 19 Basi sasa, nakusihi, bwana wangu, mfalme, na asikie maneno ya mtumishi wake. Ikiwa ni Bwana aliyekuondokesha juu yangu, na akubali sadaka; bali ikiwa ni wanadamu, na walaaniwe mbele za Bwana; kwa sababu wamenifukuza leo, nisishikamane na urithi wa Bwana, wakisema, Enenda, katumikie miungu mingine. 20 Basi sasa, isianguke damu yangu chini mbali na uso wa Bwana; maana mfalme wa Israeli ametoka ili kutafuta uhai wangu, kama vile mtu awindavyo kware mlimani. 21 Ndipo Sauli akasema, Nimekosa; rudi, Daudi, mwanangu; maana sitakudhuru tena, kwa kuwa maisha yangu yalikuwa na thamani machoni pako leo; angalia, nimetenda upumbavu, nimekosa sana. 22 Daudi akajibu, akasema, Litazame fumo hili, Ee mfalme! Kijana mmoja na avukie huku, alitwae. 23 Naye Bwana atamlipa kila mtu haki yake, na uaminifu wake; maana Bwana amekutia mikononi mwangu leo, nami nalikataa kuunyosha mkono wangu juu ya masihi wa BWANA. 24 Tena, angalia, kama vile maisha yako yalivyokuwa na thamani machoni pangu, kadhalika na maisha yangu na yawe na thamani machoni pa Bwana, akaniokoe katika shida zote. 25 Ndipo Sauli akamwambia Daudi, Ubarikiwe, Daudi, mwanangu; utatenda mambo makuu, tena hakika yako utashinda. Basi, Daudi akaenda zake; Sauli naye akarudi kwao.

1 Samweli 27

1 Ndipo Daudi aliposema moyoni mwake, Siku moja, basi, mimi nitaangamia kwa mkono wa Sauli; hakuna jema zaidi kwangu kuliko kukimbia mpaka nchi ya Wafilisti; naye Sauli atakata tamaa kwa habari yangu, asinitafute tena mipakani mwote mwa Israeli; hivyo nitaokoka katika mikono yake. 2 Basi Daudi akaondoka, yeye na hao watu mia sita aliokuwa nao, akamvukia Akishi, mwana wa Maoki, mfalme wa Gathi. 3 Daudi akakaa huko Gathi pamoja na Akishi, yeye na watu wake, kila mtu na watu wa nyumbani mwake; Daudi naye alikuwa na wakeze wawili, Ahinoamu wa Yezreeli, na Abigaili wa Karmeli, aliyekuwa mkewe Nabali. 4 Naye Sauli akaambiwa ya kwamba Daudi amekimbia mpaka Gathi; wala hakumtafuta tena. 5 Daudi akamwambia Akishi, Sasa kama nimeona kibali machoni pako na nipewe mahali katika miji hii mmojawapo mashambani, nipate kukaa huko; mbona mtumwa wako akae katika mji wa kifalme pamoja na wewe? 6 Ndipo Akishi akampa Siklagi siku ile; kwa sababu hiyo huo mji wa Siklagi ni mali ya wafalme wa Yuda hata hivi leo. 7 Na hesabu ya siku alizokaa Daudi katika nchi ya Wafilisti ilikuwa mwaka mzima na miezi minne. 8 Naye Daudi na watu wake walikuwa wakikwea na kuwashambulia Wageshuri, na Wagirizi, na Waamaleki waliokuwa wenyeji wa nchi hiyo, tangu Telemu, hapo uendapo Shuri, hata mpaka nchi ya Misri. 9 Tena Daudi akaipiga nchi hiyo, asimhifadhi hai mume wala mke, akateka nyara kondoo, na ng'ombe, na punda, na ngamia na mavazi; kisha akarejea na kufika kwa Akishi. 10 Naye Akishi humwuliza, Je! Mmeshambulia upande gani leo? Na Daudi husema, Juu ya Negebu ya Yuda, au, juu ya Negebu ya Wayerameeli, au, juu ya Negebu ya Wakeni. 11 Tena Daudi hakumhifadhi hai mume wala mke, ili kuwaleta Gathi maana alisema, Wasituchongee kusema, Ndivyo alivyofanya Daudi, tena ndivyo ilivyokuwa desturi yake wakati wote alipokaa katika nchi ya Wafilisti. 12 Hivyo Akishi akamsadiki Daudi, akasema, Amewachukiza kabisa hao watu wake Israeli; kwa hiyo atakuwa mtumishi wangu hata milele.

1 Samweli 28

1 Ikawa siku zile hao Wafilisti wakakusanya majeshi yao waende vitani, ili kupigana na Israeli. Naye Akishi akamwambia Daudi, Jua hakika ya kuwa wewe utatoka pamoja nami jeshini, wewe na watu wako. 2 Naye Daudi akamwambia Akishi, Vema, sasa utajua atakayoyatenda mtumishi wako. Naye Akishi akamwambia Daudi, Haya basi! Mimi nitakufanya wewe kuwa mlinda kichwa changu daima. 3 Basi Samweli alikuwa amefariki dunia, nao Israeli wote walikuwa wamemwomboleza, na kumzika huko Rama, ndani ya mji wake mwenyewe. Tena Sauli alikuwa amewaondolea mbali hao wenye pepo wa utambuzi na wachawi katika nchi. 4 Nao Wafilisti wakakusanyika, wakaenda kufanya kambi huko Shunemu; naye Sauli akawakusanya Waisraeli wote, nao wakapiga hema katika Gilboa. 5 Basi alipowaona hao majeshi ya Wafilisti, huyo Sauli akaogopa, na moyo wake ukatetemeka sana. 6 Lakini Sauli alipouliza kwa Bwana, Bwana hakumjibu, wala kwa ndoto, wala kwa Urimu, wala kwa manabii. 7 Ndipo Sauli akawaambia watumishi wake, Nitafutieni mwanamke mwenye pepo wa utambuzi, nipate kumwendea na kuuliza kwake. Watumishi wake wakamwambia, Tazama, yuko mwanamke mwenye pepo wa utambuzi huko Endori. 8 Basi Sauli akajigeuza, na kuvaa mavazi mengine, kisha akaenda, yeye na watu wawili pamoja naye, wakamfikilia yule mwanamke usiku; akasema, Tafadhali unibashirie kwa utambuzi, ukanipandishie yeye nitakayemtaja kwako. 9 Yule mwanamke akamwambia, Angalia, unajua alivyofanya Sauli, jinsi alivyowakatilia mbali hao wenye pepo wa utambuzi na wachawi katika nchi; mbona basi wanitegea tanzi uhai wangu, ili kuniua? 10 Naye Sauli akamwapia kwa Bwana, akasema, Aishivyo Bwana, haitakupata adhabu yo yote kwa jambo hili. 11 Ndipo yule mwanamke aliposema, Je! Ni nani nitakayekupandishia? Naye akasema, Nipandishie Samweli. 12 Hata yule mwanamke alipomwona Samweli alilia kwa sauti kuu; na yule mwanamke akamwambia Sauli, akasema, Mbona umenidanganya? Kwa kuwa wewe ndiwe Sauli. 13 Mfalme akamwambia Usiogope; waona nini? Yule mwanamke akamwambia Sauli, Naona mungu anatoka katika nchi. 14 Naye akamwuliza, Ni mfano wa nini? Akajibu, Ni mzee anazuka; naye amefunikwa vazi. Basi Sauli akatambua ya kwamba ndiye Samweli mwenyewe, akainama uso wake mpaka nchi, akasujudia. 15 Ndipo Samweli akamwambia Sauli, Mbona umenitaabisha mimi, hata kunipandisha juu? Sauli akajibu, Mimi nimetaabika sana; kwa kuwa hao Wafilisti wananifanyia vita, naye Mungu ameniacha; hanijibu tena, wala kwa manabii, wala kwa ndoto; kwa hiyo nimekuita wewe, ili wewe unijulishe nifanyeje. 16 Samweli akasema, Kwa nini kuniuliza mimi, akiwa Bwana amekuacha, naye amekuwa adui yako? 17 Yeye Bwana amekutendea kama alivyosema kwa kinywa changu; Bwana amekurarulia ufalme mkononi mwako, na kumpa jirani yako, yaani, Daudi. 18 Kwa sababu wewe hukuitii sauti ya Bwana, wala hukumtimilizia hasira yake kali juu ya Amaleki; kwa sababu hii Bwana amekutendea hili leo. 19 Tena pamoja na wewe Bwana atawatia Israeli mikononi mwa Wafilisti; hata na kesho wewe na wanao mtakuwapo pamoja nami; tena Bwana atawatia jeshi la Israeli pia mikononi mwa Wafilisti. 20 Mara Sauli akaanguka chini kifulifuli, akaingiwa na hofu kuu kwa sababu ya maneno hayo ya Samweli, wala hakuwa na nguvu yo yote; kwa maana hakula chakula mchana kutwa, wala usiku kucha. 21 Ndipo yule mwanamke akamwendea Sauli, akamwona ya kuwa yeye ametaabika sana, akamwambia, Angalia, mjakazi wako ameisikiliza sauti yako, nami nimeutia uhai wangu mkononi mwangu, nami nimeyasikiliza maneno yako uliyoniambia. 22 Basi sasa, tafadhali, wewe uisikilize sauti ya mjakazi wako, nikakuandalie ngaa mkate kidogo; ukale, ili upate nguvu, utakapokwenda zako. 23 Lakini yeye alikataa, akasema, Mimi sitaki kula. Ila watumishi wake, pamoja na yule mwanamke, wakamlazimisha; naye akaisikiliza sauti yao. Basi akainuka hapo chini, akaketi juu ya kitanda. 24 Naye yule mwanamke alikuwa na ndama aliyenona nyumbani; akafanya haraka kumchinja; akatwaa na unga, akaukanda, akafanya mkate wa mofa kwa unga huo; 25 kisha akamwandalia Sauli na watumishi wake; wakala. Ndipo wakaondoka, wakaenda zao usiku ule.

1 Samweli 29

1 Basi hao Wafilisti wakakusanya majeshi yao yote huko Afeki; nao Waisraeli wakafanya kambi karibu na chemchemi iliyoko Yezreeli. 2 Nao mashehe wa Wafilisti wakapita mbele, mia kwa mia, na elfu kwa elfu; naye Daudi na watu wake wakapita wa mwisho pamoja na Akishi. 3 Ndipo wakuu wa Wafilisti wakasema, Waebrania hawa wafanyani hapa? Naye Akishi akawaambia wakuu wa Wafilisti, Je! Siye huyu Daudi, yule mtumishi wa Sauli, mfalme wa Israeli, ambaye amefuatana na mimi siku hizi, naam, miaka hii, wala mimi nisione hatia kwake, tangu hapo aliponiangukia mimi hata leo? 4 Lakini wakuu wa Wafilisti wakamkasirikia; nao wakuu wa Wafilisti wakamwambia, Mrudishe huyu, apate kurejea mahali pake ulipomwagiza, wala asiende pamoja nasi vitani, asije akawa adui wetu vitani; kwani mtu huyu angejipatanisha na bwana wake kwa njia gani? Je! Si kwa vichwa vya watu hawa? 5 Je! Siye huyo Daudi, ambaye waliimbiana habari zake katika michezo, wakisema,Sauli amewaua elfu zake,Na Daudi makumi elfu yake? 6 Ndipo Akishi akamwita Daudi, akamwambia, Aishivyo Bwana, wewe umekuwa mwenye adili, tena kutoka kwako na kuingia kwako pamoja nami katika jeshi ni kwema machoni pangu; kwa sababu mimi sikuona uovu ndani yako tangu siku ile uliponijia hata leo; walakini hao wakuu hawakuridhii. 7 Basi sasa urudi, uende zako kwa amani, ili usiwachukize hao mashehe wa Wafilisti. 8 Naye Daudi akamwambia Akishi, Lakini mimi nimefanyaje? Nawe umeona nini kwangu mimi mtumwa wako, muda wote niliokaa mbele yako hata leo, nisipate ruhusa niende na kupigana na adui za bwana wangu mfalme? 9 Akishi akajibu, akamwambia Daudi, Mimi najua ya kuwa u mwema machoni pangu, kama malaika wa Mungu; ila hao wakuu wa Wafilisti wamesema, Huyu hatakwea pamoja nasi kwenda vitani. 10 Kwa hiyo sasa amka asubuhi na mapema, wewe na watumwa wa bwana wako waliokuja pamoja nawe; nanyi mtakapoamka asubuhi na mapema, na kupata mwanga, nendeni zenu. 11 Basi Daudi akaamka asubuhi na mapema, yeye na watu wake, kwenda zao asubuhi, kuirudia nchi ya Wafilisti. Nao Wafilisti wakakwea kwenda Yezreeli.

1 Samweli 30

1 Ikawa, Daudi na watu wake walipokuwa wamefika Siklagi siku ya tatu, hao Waamaleki walikuwa wameshambulia Negebu, na Siklagi, nao wameupiga Siklagi, na kuuchoma moto; 2 nao wamewachukua mateka wanawake waliokuwamo wakubwa kwa wadogo; hawakuwaua wo wote, ila wakawachukua, wakaenda zao. 3 Basi Daudi na watu wake walipoufikilia mji, tazama, ulikuwa umechomwa moto; na wake zao, na watoto wao, waume kwa wake, wamechukuliwa mateka. 4 Ndipo Daudi na watu waliokuwa pamoja naye wakainua sauti zao na kulia, hata walipokuwa hawana nguvu za kulia tena. 5 Na hao wake wawili wa Daudi walikuwa wamechukuliwa mateka, Ahinoamu wa Yezreeli, na Abigaili, aliyekuwa mkewe Nabali, wa Karmeli. 6 Naye Daudi akafadhaika sana; kwa sababu watu walikuwa wakisema kwamba apigwe kwa mawe, kwa maana nafsi za hao watu wote walisononeka, kila mtu kwa ajili ya wanawe na binti zake; lakini Daudi alijitia nguvu katika Bwana, Mungu wake. 7 Kisha Daudi akamwambia Abiathari, kuhani, mwana wa Ahimeleki, Tafadhali niletee hapa hiyo naivera. Naye Abiathari akamletea Daudi naivera huko. 8 Daudi akauliza kwa Bwana, akasema, Je! Nikiwafuata jeshi hili, nitawapata? Naye akamjibu, Fuata; kwa kuwa hakika utawapata, nawe hukosi utawapokonya wote. 9 Basi Daudi akaenda, yeye na wale watu mia sita waliokuwa pamoja naye, nao wakakifikilia kijito Besori, ambapo wale walioachwa nyuma walikaa. 10 Lakini Daudi akakaza kufuata, yeye na watu mia nne; kwa maana watu mia mbili walikaa nyuma, ambao walitaka kuzimia hata hawakuweza kukivuka hicho kijito Besori. 11 Nao wakamkuta Mmisri mavueni, wakamleta kwa Daudi, na kumpa chakula, naye akala; nao wakampa maji ya kunywa; 12 kisha wakampa kipande cha mkate wa tini, na vishada viwili vya zabibu; naye akiisha kula roho yake ikamrudia; kwa maana alikuwa hakula chakula wala kunywa maji, siku tatu mchana na usiku. 13 Ndipo Daudi akamwuliza, Wewe u mtu wa nani; nawe umetoka wapi? Naye akasema, Mimi ni kijana wa Misri, mtumwa wa Mwamaleki mmoja; bwana wangu aliniacha, kwa sababu tangu siku hizi tatu nalishikwa na ugonjwa. 14 Sisi tulishambulia Negebu ya Wakerethi, na ya milki ya Yuda, na Negebu ya Kalebu; na huo mji wa Siklagi tukauchoma moto. 15 Daudi akamwambia, Je! Wewe utaniongoza chini hata nilifikilie jeshi hilo? Naye akasema, Uniapie kwa Mungu, ya kwamba hutaniua, wala kunitia mikononi mwa huyo bwana wangu, nami nitakuongoza chini hata kulifikilia jeshi hilo. 16 Na hapo alipokuwa amewaongoza chini, tazama, hao walikuwa wametawanyika juu ya nchi yote, wakila na kunywa, na kufanya karamu, kwa sababu ya hizo nyara kubwa walizochukua katika nchi ya Wafilisti, na katika nchi ya Yuda. 17 Naye Daudi akawapiga tangu ukungu wa jioni hata jioni ya siku ya pili; hakuna aliyeokoka, ila vijana mia nne waliopanda ngamia na kukimbia. 18 Daudi akawapokonya wote waliokuwa wamechukuliwa na Waamaleki; naye Daudi akawaokoa wakeze wawili. 19 Wala hawakupotewa na kitu, mdogo wala mkubwa, wana wala binti, nyara wala cho chote walichojitwalia hao; Daudi akavirudisha vyote. 20 Naye Daudi akatwaa makundi yote ya kondoo na ng'ombe, ambao waliwatanguliza mbele ya wanyama wale wengine, wakasema, Hao ndio nyara za Daudi. 21 Kisha Daudi aliwafikilia wale watu mia mbili, waliokuwa wametaka kuzimia, hata wasiweze kumfuata Daudi, wale waliowaacha wakae karibu na kijito cha Besori; nao wakatoka nje ili kumlaki Daudi, na kuwalaki hao watu waliokuwa pamoja naye, naye Daudi alipowakaribia hao watu, aliwasalimu. 22 Ndipo watu waovu wote na wale wasiofaa, miongoni mwa hao waliokwenda pamoja na Daudi, wakasema, Kwa kuwa watu hawa hawakuenda pamoja na sisi, hatutawapa kitu cho chote katika hizo nyara tulizozitwaa tena, isipokuwa kila mtu atapewa mkewe na watoto wake, wawachukue na kwenda zao. 23 Ndipo Daudi akasema, La, ndugu zangu, msitende hivyo katika hizo nyara alizotupa Bwana, ambaye ndiye aliyetuhifadhi, akalitia mikononi mwetu lile jeshi lililokuja kinyume chetu. 24 Tena ni nani atakayewasikiliza ninyi katika jambo hili? Kwa kuwa kama lilivyo fungu lake yeye ashukaye vitani, ndivyo litakavyokuwa na fungu lake huyo akaaye karibu na vyombo; watagawiwa sawasawa. 25 Basi ikawa hivyo tangu siku ile na baadaye; akaiweka iwe amri na agizo la Israeli hata leo. 26 Basi Daudi alipofika Siklagi, aliwapelekea wazee wa Yuda, rafiki zake, sehemu ya nyara, akasema, Angalieni, zawadi yenu katika nyara za adui za Bwana; 27 yaani, kwa hao wa Betheli, na kwa hao wa Ramoth-Negebu, na kwa hao wa Yatiri; 28 na kwa hao wa Aroeri, na kwa hao wa Sifmothi, na kwa hao wa Eshtemoa; 29 na kwa hao wa Rakali, na kwa hao wa miji ya Wayerameeli, na kwa hao wa miji ya Wakeni; 30 na kwa hao wa Horma, na kwa hao wa Korashani, na kwa hao wa Athaki; 31 na kwa hao wa Hebroni, na kwa hao wa kila mahali alipozoelea Daudi mwenyewe na watu wake.

1 Samweli 31

1 Basi Wafilisti wakapigana na Israeli; nao watu wa Israeli wakakimbia mbele ya Wafilisti, wakaanguka wameuawa katika mlima wa Gilboa. 2 Wafilisti wakamfuatia sana Sauli na wanawe, Wafilisti wakawaua Yonathani, na Abinadabu, na Malkishua, wana wa Sauli. 3 Tena vita vilikuwa vikali sana juu ya Sauli, na wapiga upinde wakampata; hata akafadhaika sana kwa sababu ya wapiga upinde. 4 Ndipo Sauli akamwambia yule mchukua silaha zake, Futa upanga wako, unichome nao; wasije watu hawa wasiotahiriwa wakanichoma, na kunisimanga. Lakini huyo mchukua silaha zake akakataa; kwa sababu aliogopa sana. Basi Sauli akautwaa upanga wake, akauangukia. 5 Na mchukua silaha zake alipoona ya kuwa Sauli amekufa, yeye naye akauangukia upanga wake, akafa pamoja naye. 6 Hivyo Sauli akafa, na wanawe watatu, na mchukua silaha zake, na watu wake wote pamoja siku iyo hiyo. 7 Kisha watu wa Israeli waliokuwa upande wa pili wa bonde lile, na ng'ambo ya Yordani, walipoona ya kuwa watu wa Israeli wamekimbia, na ya kuwa Sauli na wanawe wamekufa, wakaiacha miji yao, wakakimbia; nao Wafilisti wakaenda wakakaa humo. 8 Hata ikawa, siku ya pili yake, Wafilisti walipokwenda kuwateka nyara waliouawa, walimwona Sauli na wanawe watatu wameanguka juu ya mlima wa Gilboa. 9 Wakamkata kichwa, wakamvua silaha zake, wakapeleka wajumbe kwenda nchi ya Wafilisti pande zote, ili kutangaza habari nyumbani mwa sanamu zao, na kwa watu. 10 Wakaziweka silaha zake nyumbani mwa Maashtorethi; wakakitundika kiwiliwili chake katika ukuta wa Beth-shani. 11 Na wenyeji wa Yabesh-Gileadi waliposikia habari zake, jinsi hao Wafilisti walivyomtenda Sauli, 12 wakainuka mashujaa wote, wakaenda usiku kucha, wakautwaa mwili wake Sauli, na miili ya wanawe, na kuiondoa ukutani kwa Beth-shani nao wakaja Yabeshi, na kuiteketeza huko. 13 Kisha wakaitwaa mifupa yao, na kuizika chini ya mkwaju huko Yabeshi, nao wakafunga siku saba.

2 Samweli 1

1 Ikawa baada ya kufa kwake Sauli, hapo Daudi aliporudi katika kuwaua Waamaleki, naye Daudi amekaa siku mbili katika Siklagi; 2 hata siku ya tatu ikawa, tazama! Akaja mtu kutoka kambi ya Sauli, nguo zake zimeraruliwa, tena ana mavumbi kichwani mwake; basi, ikawa alipomfikia Daudi, akaanguka chini, akamsujudia. 3 Daudi akamwambia, Umetoka wapi? Akamwambia, Nimeokoka katika kambi ya Israeli. 4 Daudi akamwambia, Yalikwendaje? Tafadhali uniambie. Akajibu, Watu wamekimbia vitani, tena watu wengi wameanguka wamekufa; hata Sauli naye na Yonathani, mwanawe, wamekufa. 5 Daudi akamwambia yule kijana aliyempa habari, Umejuaje ya kuwa Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa? 6 Yule kijana aliyempa habari akasema, Nalikuwapo kwa nasibu juu ya kilima cha Gilboa, na tazama, Sauli alikuwa ameegemea fumo lake; na tazama, magari na wapanda farasi wanamfuatia kwa kasi. 7 Naye alipotazama nyuma, akaniona, akaniita. Nikajibu, Mimi hapa. 8 Akaniambia, U nani wewe? Nikamjibu, Mimi ni Mwamaleki. 9 Akaniambia, Tafadhali simama karibu nami, ukaniue, maana shida imenipata; kwa sababu roho yangu ingali hai ndani yangu. 10 Basi, nikasimama karibu naye, nikamwua, kwa sababu nalijua hakika ya kuwa hawezi kupona baada ya kuanguka; kisha nikaitwaa ile taji iliyokuwa kichwani mwake, na kikuku kilichokuwa mkononi mwake, nami nimevileta hapa kwa bwana wangu. 11 Ndipo Daudi akashika nguo zake akazirarua na kadhalika watu wote waliokuwa pamoja naye; 12 wakaomboleza, wakalia, wakafunga hata jioni, kwa ajili ya Sauli, na kwa ajili ya Yonathani mwanawe, na kwa ajili ya watu wa Bwana na kwa ajili ya nyumba ya Israeli; kwa sababu wameanguka kwa upanga. 13 Naye Daudi akamwambia yule kijana aliyempa habari, Watoka wapi wewe? Akajibu, Mimi ni mwana wa mgeni, Mwamaleki. 14 Daudi akamwambia, Jinsi gani hukuogopa kuunyosha mkono wako umwangamize masihi wa BWANA? 15 Ndipo Daudi akamwita mmoja wa vijana, akamwambia, Mwendee, ukamwangukie. Basi akampiga hata akafa. 16 Daudi akamwambia, Damu yako na iwe juu ya kichwa chako mwenyewe; maana umejishuhudia nafsi yako ukisema, Nimemwua masihi wa Bwana. 17 Basi Daudi akamwomboleza Sauli, na Yonathani, mwanawe, maombolezo haya; 18 (kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Yashari), akasema, Wana wa Yuda na wafundishwe haya, 19 Walio fahari yako, Ee Israeli Juu ya mahali pako palipoinuka wameuawa; Jinsi mashujaa walivyoanguka! 20 Msiyahubiri mambo haya katika Gathi, Msiyatangaze katika njia za Ashkeloni; Wasije wakashangilia binti za Wafilisti, Binti za wasiotahiriwa wakasimanga. 21 Enyi milima ya Gilboa, visiwepo juu yenu Umande wala mvua, wala mashamba ya matoleo; Maana ndipo ilipotupwa kwa aibu ngao ya shujaa, Ngao yake Sauli, pasipo kutiwa mafuta. 22 Kutoka kwa damu yao waliouawa, Kutoka kwa shahamu yao mashujaa, Upinde wa Yonathani haukurudi nyuma, Wala upanga wa Sauli haukurudi bure. 23 Sauli na Yonathani walipendwa na kupendeza Maishani wala mautini hawakutengwa; Walikuwa wepesi kuliko tai, Walikuwa hodari kuliko simba. 24 Enyi binti za Israeli, mlilieni Huyo Sauli, ambaye aliwavika Mavazi mekundu kwa anasa, Akazipamba nguo zenu dhahabu. 25 Jinsi mashujaa walivyoanguka Katikati ya vita! Ee Yonathani, wewe umeuawa Juu ya mahali pako palipoinuka 26 Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani, ndugu yangu, Ulikuwa ukinipendeza sana; Upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu, Kupita upendo wa wanawake. 27 Jinsi mashujaa walivyoanguka, Na silaha za vita zilivyoangamia!

2 Samweli 2

1 Ikawa baada ya hayo, Daudi akauliza kwa Bwana, akasema, Je! Niupandie mji wo wote wa Yuda? Bwana akamwambia, Haya! Panda. Daudi akasema, Niupandie mji upi? Akasema, Hebroni. 2 Basi Daudi akapanda aende huko, pamoja na wakeze wawili, Ahinoamu wa Yezreeli, na Abigaili, mkewe Nabali, wa Karmeli. 3 Daudi naye akawapandisha watu wake waliokuwa pamoja naye, kila mtu na watu wa nyumbani mwake; wakakaa katika miji ya Hebroni. 4 Basi watu wa Yuda wakaenda, wakamtia Daudi mafuta huko, awe mfalme juu ya nyumba ya Yuda. Wakamwambia Daudi wakasema, Watu wa Yabesh-gileadi ndio waliomzika Sauli. 5 Basi Daudi akatuma wajumbe kwa watu wa Yabesh-gileadi, na kuwaambia, Na mbarikiwe ninyi na Bwana, kwa kuwa mmemtendea bwana wenu fadhili hii, yaani Sauli, mkamzika. 6 Bwana naye sasa awatendee ninyi fadhili na kweli; mimi nami nitawalipeni fadhili hiyo, kwa sababu mmetenda jambo hilo. 7 Basi sasa, mikono yenu na itiwe nguvu, nanyi iweni mashujaa; maana Sauli, bwana wenu, amekufa, tena nyumba ya Yuda wamenitia mimi mafuta niwe mfalme juu yao. 8 Basi Abneri, mwana wa Neri, amiri wa jeshi la Sauli, alikuwa amemtwaa Ishboshethi, mwana wa Sauli, na kumvusha na kumpeleka Mahanaimu; 9 akamweka awe mfalme juu ya Gileadi, na Waasheri, na Yezreeli, na Efraimu, na Benyamini, na juu ya Israeli wote. 10 (Huyo Ishboshethi, mwana wa Sauli, umri wake alikuwa amepata miaka arobaini alipoanza kutawala juu ya Israeli, akatawala miaka miwili.) Lakini nyumba ya Yuda waliandamana na Daudi. 11 Na wakati Daudi alipotawala Hebroni juu ya nyumba ya Yuda ulikuwa miaka saba na miezi sita. 12 Basi Abneri, mwana wa Neri, na watumishi wa Ishboshethi, mwana wa Sauli, wakatoka Mahanaimu kwenda Gibeoni. 13 Huyo Yoabu naye, mwana wa Seruya, na watumishi wa Daudi, wakatoka, wakakutana nao karibu na ziwa la Gibeoni; wakaketi, hawa upande huu wa ziwa, na hawa upande huu wa ziwa. 14 Abneri akamwambia Yoabu, Tafadhali vijana hawa na waondoke na kucheza mbele yetu. Yoabu akasema, Haya! Na waondoke. 15 Basi wakaondoka, wakaenda upande wa pili kwa hesabu yao watu kumi na wawili wa Benyamini, na wa Ishboshethi, mwana wa Sauli na watu kumi na wawili wa watumishi wa Daudi. 16 Wakakamatana, kila mtu akimshika mwenziwe kichwa chake, na kutia upanga wake katika ubavu wa mwenzake; wakaanguka pamoja; hata mahali pale pakaitwa Helkath-hasurimu, napo ni katika Gibeoni. 17 Vita vile vilikuwa vikali sana siku ile; naye Abneri akashindwa, na watu wa Israeli, mbele ya watumishi wa Daudi. 18 Na wana watatu wa Seruya walikuwako huko, Yoabu, na Abishai, na Asaheli; na Asaheli alikuwa mwepesi wa miguu kama kulungu. 19 Naye Asaheli akamfuatia Abneri; na katika kwenda kwake hakugeuka kwenda mkono wa kuume wala mkono wa kushoto katika kumfuatia Abneri. 20 Basi Abneri akatazama nyuma yake, akasema, Ni wewe, Asaheli? Akajibu, Ni mimi. 21 Basi Abneri akamwambia, Geuka mkono wa kuume au mkono wa kushoto, ukamshike mmoja wa vijana, ukazitwae silaha zake. Lakini Asaheli hakukubali kugeuka na kuacha kumfuata. 22 Abneri akamwambia Asaheli mara ya pili, Geuka, acha kunifuatia mimi; kwa nini nikupige hata chini? Hapo ningewezaje kuinua uso wangu mbele ya Yoabu, ndugu yako? 23 Lakini akakataa kugeuka; kwa hiyo Abneri akampiga tumboni kwa ncha ya nyuma ya mkuki wake, ule mkuki ukamtoka kwa nyuma; naye akaanguka hapo, akafa papo hapo; ikawa, watu wote waliofika hapo, alipoanguka Asaheli na kufa, wakasimama. 24 Ila Yoabu na Abishai wakamfuatia Abneri; na jua likachwa hapo walipoufikilia mlima wa Ama, uelekeao Gia, katika njia ya nyika ya Gibeoni. 25 Nao wana wa Benyamini wakakusanyika pamoja nyuma ya Abneri, wakawa kikosi kimoja, wakasimama juu ya mlima. 26 Ndipo huyo Abneri akamwita Yoabu, akasema, Je! Upanga uwale watu sikuzote? Je! Hujui ya kwamba utakuwa uchungu mwisho wake? Basi itakuwa hata lini usijewaamuru watu warudi na kuacha kuwafuatia ndugu zao? 27 Naye Yoabu akasema, Aishivyo Mungu, usingalinena, basi asubuhi wangalikwenda zao, wasiwafuatie kila mtu ndugu yake. 28 Basi Yoabu akapiga tarumbeta, na watu wote wakasimama, wasiwafuatie Israeli tena, wala hawakupigana tena. 29 Wakaenda Abneri na watu wake usiku ule wote kati ya ile Araba; wakavuka Yordani, wakapita kati ya Bithroni yote, wakaja Mahanaimu. 30 Akarudi Yoabu naye kutoka kumfuatia Abneri; na alipokwisha kuwakusanya watu wote pamoja, wa hao watumishi wa Daudi walipungukiwa na watu kumi na kenda pamoja na Asaheli. 31 Ila watumishi wa Daudi walikuwa wamewapiga watu wa Benyamini, na watu wa Abneri, hata wakafa watu mia tatu na sitini. 32 Nao wakamwinua Asaheli, wakamzika katika kaburi la baba yake, lililokuwako Bethlehemu. Yoabu na watu wake wakaenda usiku kucha, wakapambazukiwa huko Hebroni.

2 Samweli 3

1 Basi kulikuwa na vita siku nyingi kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi; Daudi akaendelea akasitawi, lakini nyumba ya Sauli ikaendelea kudhoofika. 2 Naye Daudi akazaliwa wana huko Hebroni; mzaliwa wake wa kwanza alikuwa Amnoni, wa Ahinoamu wa Yezreeli; 3 na wa pili wake Danieli, wa Abigaili mkewe Nabali wa Karmeli; na wa tatu Absalomu, mwana wa Maaka binti Talmai, mfalme wa Geshuri, 4 na wa nne Adoniya, mwana wa Hagithi; na wa tano Shefatia, mwana wa Abitali; 5 na wa sita Ithreamu, wa Egla, mkewe Daudi. Hawa walizaliwa kwa Daudi huko Hebroni. 6 Ikawa, wakati vilipokuwapo vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi, Abneri akajipatia nguvu nyumbani kwa Sauli. 7 Basi Sauli alikuwa na suria, jina lake akiitwa Rispa, binti Aya; Ishboshethi akamwuliza Abneri, Kwa nini umeingia kwa suria ya babangu? 8 Basi Abneri akakasirika kwa maneno ya Ishboshethi, akasema, Je! Mimi ni kichwa cha mbwa, aliye wa Yuda? Hata leo hivi nawafanyia fadhili nyumba ya Sauli babako, na ndugu zake, na rafiki zake, nisikutie wewe mkononi mwa Daudi; nawe hata hivyo wanitia hatiani leo kwa mwanamke huyu. 9 Mungu amfanyie Abneri vivyo, na kuzidi, nisipomtendea Daudi kama vile Bwana alivyomwapia; 10 kuupitisha ufalme toka nyumba ya Sauli, na kukisimamisha kiti cha Daudi juu ya Israeli, na juu ya Yuda, toka Dani mpaka Beer-sheba. 11 Wala hakuweza kumjibu Abneri tena, kwa sababu alimwogopa. 12 Basi Abneri akatuma wajumbe kwa Daudi mahali alipokuwapo, akisema, Nchi hii ni ya nani? Fanya agano nami, na tazama, mkono wangu utakuwa pamoja nawe, ili kuwaleta Israeli wote kwako. 13 Daudi akasema, Vema, nitafanya agano nawe, lakini nina sharti moja nitakalo kwako, nalo ni hili; Hutaniona uso wangu, isipokuwa uniletee Mikali, binti Sauli, hapo ujapo kuniona uso wangu. 14 Basi Daudi akatuma wajumbe kwa Ishboshethi, mwana wa Sauli, kusema, Nipe mke wangu Mikali, niliyemposa kwa govi mia za Wafilisti. 15 Basi Ishboshethi akatuma watu, akamnyang'anya Paltieli, mwana wa Laishi, mumewe, mwanamke huyo. 16 Huyo mumewe akafuatana naye, akiendelea na kulia, akamfuata mpaka Bahurimu. Ndipo Abneri akamwambia, Haya, rudi. Naye akarudi. 17 Basi Abneri akafanya mashauri na wazee wa Israeli, akasema, Zamani mlitaka Daudi awamiliki; 18 basi, sasa, fanyeni hayo; kwa maana Bwana amemtaja Daudi, akisema, kwa mkono wa mtumishi wangu, Daudi, nitawaokoa watu wangu Israeli katika mikono ya Wafilisti, na katika mikono ya adui zao wote. 19 Tena Abneri alinena masikioni mwa Benyamini; kisha Abneri akaenda ili kunena masikioni mwa Daudi huko Hebroni maneno yote yaliyoonekana kuwa mema machoni pa Israeli, na machoni pa nyumba yote ya Benyamini. 20 Basi Abneri akamwendea Daudi huko Hebroni, na watu ishirini pamoja naye. Daudi akamfanyia karamu Abneri, na watu wote waliokuwa pamoja naye. 21 Kisha Abneri akamwambia Daudi, Nitaondoka, niende zangu; nami nitamkusanyia bwana wangu mfalme Israeli wote, ili wafanye agano nawe, ukamiliki juu ya wote inaowatamani roho yako. Basi Daudi akamruhusu Abneri; naye akaenda zake kwa amani. 22 Na tazama, watumishi wa Daudi pamoja na Yoabu walitoka jeshini, wakaleta mateka mengi pamoja nao; lakini Abneri hakuwako Hebroni kwa Daudi; maana alikuwa amemruhusu, naye amekwisha kwenda zake kwa amani. 23 Hata Yoabu, na jeshi lote waliokuwa pamoja naye, walipofika, watu wakamwambia Yoabu, wakisema, Abneri, mwana wa Neri, alikuja kwa mfalme, naye amemruhusu, naye amekwenda zake kwa amani. 24 Basi Yoabu akamwendea mfalme, akasema, Umefanyaje? Tazama, Abneri amekuja kwako; mbona umemruhusu, naye amekwisha kwenda zake? 25 Wewe wamjua Abneri, mwana wa Neri, ya kuwa alikuja ili kukudanganya, apate kujua kutoka kwako, na kuingia kwako, akajue yote uyatendayo. 26 Naye Yoabu alipotoka kwa Daudi, akapeleka wajumbe kumfuata Abneri, wakamrudisha kutoka kisima cha Sira; lakini Daudi alikuwa hana habari. 27 Basi Abneri alipokuwa amerudi Hebroni, Yoabu akamchukua kando hata katikati ya lango, ili aseme naye kwa faragha; akampiga mkuki wa tumbo huko, hata akafa; kwa ajili ya damu ya Asaheli, ndugu yake. 28 Hata baadaye Daudi aliposikia, akasema, Mimi na ufalme wangu hatuna hatia milele mbele za Bwana, kwa sababu ya damu ya Abneri, mwana wa Neri; 29 na imwangukie Yoabu kichwani pake, na nyumba yote ya babaye, tena hiyo nyumba ya Yoabu isikose kuwa na mtu mwenye kutoka damu, au aliye na ukoma, au mwenye kutegemea fimbo, au mwenye kuanguka kwa upanga au mwenye kuhitaji chakula. 30 Basi Yoabu, na Abishai nduguye, walimwua Abneri, kwa sababu yeye alimwua ndugu yao Asaheli katika vita huko Gibeoni. 31 Kisha Daudi alimwambia Yoabu, na watu wote waliokuwa pamoja naye, Rarueni nguo zenu, mkajivike nguo za magunia, mkamlilie Abneri. Naye mfalme Daudi akaifuata jeneza. 32 Wakamzika Abneri katika Hebroni; naye mfalme akapaza sauti yake, akalia kaburini kwa Abneri, nao watu wote wakalia. 33 Ndipo mfalme akamwomboleza Abneri, akasema, Ilimpasaje Abneri kufa afavyo mpumbavu? 34 Mikono yako haikufungwa, Wala miguu yako haikutiwa pingu; Aangukavyo mtu mbele ya wana wa uovu, ndivyo ulivyoanguka. Na watu wote wakaongeza kumlilia. 35 Wakaja na watu wote wamshurutishe Daudi kula chakula, ukalipo bado mchana; lakini Daudi akaapa, akasema Mungu anitendee vivyo, na kuzidi, nikionja mkate, au kingine cho chote kabla lichwapo jua. 36 Wakaangalia watu wote, yakawa mema machoni pao; kama yalivyokuwa mema machoni pao yote aliyoyatenda mfalme. 37 Wakajua watu wote, na Israeli wote, siku ile, ya kuwa si nia ya mfalme kwamba auawe Abneri, mwana wa Neri. 38 Kisha mfalme akawaambia watumishi wake, Hamjui ya kuwa mkuu mmoja, naye ni mtu mkubwa ameanguka leo katika Israeli? 39 Nami leo nimedhoofika, hata nijapotiwa mafuta niwe mfalme; na watu hao, wana wa Seruya, ni wagumu kwangu mimi; Bwana amlipie mwovu sawasawa na uovu wake.

2 Samweli 4

1 Hata Ishboshethi mwana wa Sauli aliposikia ya kuwa Abneri amekufa huko Hebroni, mikono yake ilikuwa dhaifu, na Waisraeli wote wakataabika. 2 Na huyo mwana wa Sauli alikuwa na watu wawili, maakida wa vikosi; jina lake mmoja akiitwa Baana, na jina la wa pili Rekabu wana wa Rimoni, Mbeerothi, wa wana wa Benyamini; (kwa maana Beerothi umehesabiwa kuwa wa Benyamini; 3 na hao Wabeerothi walikimbia kwenda Githaimu, ndipo wanapokaa hali ya ugeni hata hivi leo.) 4 Naye Yonathani, mwana wa Sauli alikuwa na mwana aliyekuwa na kilema cha miguu. Alikuwa amepata miaka mitano, habari za Sauli na Yonathani zilipofika Yezreeli, na yaya wake akamchukua akakimbia ikawa, alipokimbia kwa haraka, huyo mtoto akaanguka, akawa kilema. Na jina lake aliitwa Mefiboshethi. 5 Na wale wana wa Rimoni, Mbeerothi, Rekabu na Baana, wakaenda wakafika nyumbani kwa Ishboshethi, wakati wa hari ya mchana, alipokuwa akipumzika adhuhuri. 6 Wakafikia kati ya nyumba, kana kwamba wanataka kuchukua ngano, wakampiga mkuki wa tumbo; kisha Rekabu na Baana nduguye wakakimbia. 7 Basi walipoingia katika ile nyumba, alipokuwa amelala kitandani mwake, katika chumba chake cha kulala, wakampiga, wakamwua, wakamkata kichwa, wakachukua kichwa chake, wakaenda zao kwa njia ya Araba usiku kucha. 8 Wakamletea Daudi kichwa cha Ishboshethi huko Hebroni, wakamwambia mfalme, Tazama, hiki ni kichwa cha Ishboshethi, mwana wa Sauli, adui yako, aliyekutafuta roho yako; Bwana amemlipia kisasi bwana wangu mfalme hivi leo, juu ya Sauli, na juu ya wazao wake. 9 Naye Daudi akawajibu Rekabu na Baana, nduguye, wana wa Rimoni, Mbeerothi, akawaambia, Aishivyo Bwana, aliyenihifadhi roho yangu katika shida zote, 10 mtu mmoja aliponiambia, akasema, Tazama, Sauli amekufa, akidhani ya kuwa ameleta habari njema, nalimshika, nikamwua, huko Siklagi, ndio ujira niliompa kwa habari zake. 11 Basi, iwapo watu waovu wamemwua mtu mwenye haki kitandani mwake, je! Sasa nisitake zaidi damu yake mikononi mwenu, na kuwaondoa ninyi katika nchi? 12 Ndipo Daudi akawaagiza vijana wake, wakawaua, wakawakata mikono na miguu, wakawatundika kando ya ziwa katika Hebroni. Nao wakakitwaa kichwa cha Ishboshethi wakakizika katika kaburi la Abneri huko Hebroni.

2 Samweli 5

1 Ndipo kabila zote za Israeli wakamwendea Daudi huko Hebroni, wakasema naye, wakinena, Tazama, sisi tu mfupa wako na nyama yako. 2 Zamani za kale, hapo Sauli alipokuwa mfalme juu yetu, wewe ndiwe uliyewaongoza Israeli watoke nje, na kuingia ndani. Naye Bwana akakuambia, Wewe utawalisha watu wangu Israeli, nawe utakuwa mkuu juu ya Israeli. 3 Basi wazee wote wa Israeli wakamwendea mfalme huko Hebroni, naye mfalme Daudi akapatana nao huko Hebroni mbele za Bwana; wakamtia Daudi mafuta awe mfalme juu ya Israeli. 4 Daudi alikuwa amepata miaka thelathini alipoanza kutawala, akatawala miaka arobaini. 5 Huko Hebroni alitawala miaka saba na miezi sita; na katika Yerusalemu alitawala miaka thelathini na tatu juu ya Israeli wote na Yuda. 6 Kisha mfalme na watu wake wakaenda Yerusalemu ili kupigana na Wayebusi, wenyeji wa nchi ile; hao ndio waliomwambia Daudi, wakisema, Usipowaondoa vipofu, na viwete, hutaingia humu kamwe; huku wakidhania ya kuwa Daudi hawezi kuingia humo. 7 Lakini Daudi aliipiga ngome ya Sayuni; huu ndio mji wa Daudi. 8 Naye Daudi alisema siku hiyo, Yeye atakayewapiga Wayebusi, na apande kwenye mfereji wa maji, na kuwapiga viwete, na hao vipofu, ambao roho yake Daudi inawachukia. Kwa sababu hii watu husema, Wako vipofu na viwete hawawezi kuingia nyumbani. 9 Basi Daudi akakaa ndani ya ngome hiyo, akaiita mji wa Daudi. Kisha Daudi akajenga toka Milo na pande za ndani. 10 Naye Daudi akazidi kuwa mkuu; kwa maana Bwana, Mungu wa majeshi, alikuwa pamoja naye. 11 Kisha Hiramu, mfalme wa Tiro, akatuma wajumbe kwa Daudi, akampelekea na mierezi, na maseremala, na waashi; nao wakamjengea Daudi nyumba. 12 Akajua Daudi ya kwamba Bwana amemweka imara awe mfalme juu ya Israeli, na ufalme wake ameutukuza kwa ajili ya watu wake, Israeli. 13 Naye Daudi akazidi kujitwalia masuria na wake huko Yerusalemu baada ya kutoka Hebroni; wakazaliwa zaidi kwa Daudi wana na binti. 14 Na haya ndiyo majina ya hao waliozaliwa kwake huko Yerusalemu; Shamua, na Shobabu, na Nathani, na Sulemani, 15 na Ibhari, na Elishua; na Nefegi, na Yafia; 16 na Elishama, na Eliada, na Elifeleti. 17 Na hao Wafilisti waliposikia kwamba wamemtia Daudi mafuta ili awe mfalme juu ya Israeli, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akapata habari, akashuka akaenda ngomeni. 18 Basi Wafilisti walikuwa wamekuja na kujitawanya bondeni mwa Warefai. 19 Basi Daudi akauliza kwa Bwana, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti? Utawatia mkononi mwangu? Naye Bwana akamwambia Daudi, Panda; kwa kuwa hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako. 20 Basi Daudi akaja Baal-perasimu, naye Daudi akawapiga huko; akasema, Bwana amewafurikia adui zangu mbele yangu, kama mafuriko ya maji. Basi akapaita mahali pale Baal-perasimu. 21 Nao wakaziacha sanamu zao huko, na Daudi na watu wake wakaziondolea mbali. 22 Lakini wakapanda hao Wafilisti tena mara ya pili, wakajitawanya bondeni mwa Warefai. 23 Naye Daudi alipouliza kwa Bwana, alisema, Usipande; zunguka nyuma yao, ukawajie huko mbele ya miforsadi. 24 Kisha itakuwa, hapo utakapoisikia sauti ya kwenda katika vilele vya miforsadi, ndipo nawe ujitahidi; kwa maana ndipo Bwana ametoka mbele yako awapige jeshi la Wafilisti. 25 Ndivyo alivyotenda Daudi, vile vile kama Bwana alivyomwagiza; naye akawapiga Wafilisti toka Geba hata ujapo Gezeri.

2 Samweli 6

1 Basi Daudi akakusanya tena wateule wote wa Israeli, watu thelathini elfu. 2 Akaondoka Daudi akaenda pamoja na watu wote waliokuwa naye, mpaka Baala wa Yuda, ili kulipandisha kutoka huko sanduku la Mungu lililoitwa kwa jina, naam, jina la Bwana wa majeshi akaaye juu ya makerubi. 3 Wakaliweka sanduku la Mungu juu ya gari jipya, wakalitoa katika nyumba ya Abinadabu, iliyoko kilimani; nao Uza na Ahio wana wa Abinadabu wakaliendesha lile gari jipya. 4 Wakalitoa katika nyumba ya Abinadabu iliyoko kilimani, pamoja na sanduku la Bwana; na huyo Ahio akatangulia mbele ya sanduku. 5 Daudi na nyumba yote ya Israeli wakacheza mbele za Bwana kwa nguvu zao zote, kwa nyimbo, na kwa vinubi, na kwa vinanda, na kwa matari, na kwa kayamba, na kwa matoazi. 6 Hata walipofika kwa uga ya Nakoni, Uza akalinyoshea mkono sanduku la Mungu, akalikamata kwa maana wale ng'ombe walikunguwaa. 7 Ndipo hasira ya Bwana ikawaka juu ya Uza; naye Mungu akampiga huko kwa kosa lake; hata akafa pale pale penye sanduku la Mungu. 8 Daudi akaona uchungu kwa kuwa Bwana amemfurikia Uza; akapaita mahali pale Peres-uza hata leo. 9 Naye Daudi akamwogopa Bwana siku ile; akasema, Litanijiaje sanduku la Bwana? 10 Basi Daudi hakutaka kulileta sanduku la Bwana kwake mjini mwa Daudi; ila Daudi akalihamisha nyumbani kwa Obed-edomu, Mgiti. 11 Sanduku la Bwana akalitia katika nyumba ya Obed-edomu, Mgiti, muda wa miezi mitatu; naye Bwana akambarikia Obed-edomu, na nyumba yake yote. 12 Kisha mfalme Daudi akaambiwa ya kwamba, Bwana ameibarikia nyumba ya Obed-edomu, na vitu vyote alivyo navyo kwa ajili ya sanduku la Mungu. Daudi akaenda, akalileta sanduku la Mungu, toka nyumba ya Obed-edomu mpaka mji wa Daudi, kwa shangwe. 13 Hata ikawa, watu waliolichukua sanduku la Bwana walipokwisha kwenda hatua sita, akachinja ng'ombe na kinono. 14 Daudi akacheza mbele za Bwana kwa nguvu zake zote; na Daudi alikuwa amevaa naivera ya kitani. 15 Basi Daudi na nyumba yote ya Israeli wakalileta sanduku la Bwana kwa shangwe, na kwa sauti ya tarumbeta. 16 Ikawa, sanduku la Bwana lilipoingia mji wa Daudi Mikali, binti Sauli, akachungulia dirishani, akamwona mfalme Daudi akiruka-ruka na kucheza mbele za Bwana; akamdharau moyoni mwake. 17 Wakaliingiza sanduku la Bwana, na kuliweka mahali pake, katikati ya hema aliyoipiga Daudi kwa ajili yake, naye Daudi akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani mbele za Bwana. 18 Kisha Daudi alipokwisha kutoa sadaka ya kuteketezwa na sadaka za amani akawabarikia watu kwa jina la Bwana wa majeshi. 19 Akawagawia watu wote, mkutano wote wa Israeli, wanaume kwa wanawake, kila mtu mkate wa ngano, na kipande cha nyama, na mkate wa zabibu. Basi watu wote wakaenda zao, kila mtu nyumbani kwake. 20 Ndipo Daudi akarudi ili awabarikie watu wa nyumbani mwake. Na Mikali, binti Sauli, akatoka nje aende kumlaki Daudi, naye akasema, Mfalme wa Israeli alikuwa mtukufu leo namna gani, akijifunua mwili wake mbele ya vijakazi vya watumishi wake, mfano wa watu baradhuli mmojawapo, ajifunuavyo mwili wake mbele ya watu, asipokuwa na haya! 21 Daudi akamwambia Mikali, Ilikuwa mbele za Bwana, aliyenichagua mimi juu ya baba yako, na juu ya nyumba yake, ili kuniweka niwe mkuu juu ya watu wa Bwana, juu ya Israeli; kwa hiyo mimi nitacheza mbele za Bwana. 22 Kisha nitakuwa hafifu zaidi, nami nitakuwa mnyonge machoni pangu mimi mwenyewe; lakini kwa wale vijakazi uliowanena, kwao nitaheshimiwa. 23 Basi Mikali, binti Sauli, hakuwa na mtoto hata siku ya kufa kwake.

2 Samweli 7

1 Ikawa, mfalme alipokuwa akikaa katika nyumba yake, hapo Bwana alipomstarehesha, asiudhiwe na adui zake waliomzunguka pande zote, 2 mfalme akamwambia Nathani, nabii, Angalia sasa, mimi ninakaa katika nyumba ya mierezi, bali sanduku la Mungu linakaa ndani ya mapazia. 3 Nathani akamwambia mfalme, Haya, fanya yote yaliyomo moyoni mwako; maana Bwana yu pamoja nawe. 4 Ikawa usiku uo huo, neno la Bwana likamfikia Nathani kusema, 5 Enenda, ukamwambie mtumishi wangu, Daudi, Bwana asema hivi, Je! Wewe utanijengea nyumba, nikae ndani yake? 6 Kwa maana mimi sikukaa ndani ya nyumba, tangu siku ile niliyowatoa wana wa Israeli katika Misri, hata leo, lakini nimekaa katika hema na maskani. 7 Mahali mwote nilimokwenda na wana wa Israeli wote, je! Nimesema neno lo lote na mtu ye yote wa waamuzi wa Israeli, niliyemwagiza kuwalisha watu wangu Israeli, nikisema, Mbona hamkunijengea nyumba ya mierezi? 8 Basi, sasa, mwambie mtumishi wangu, Daudi, maneno haya, Bwana wa majeshi asema hivi, Nalikutwaa katika zizi la kondoo, katika kuwaandama kondoo, ili uwe mkuu juu ya watu wangu, juu ya Israeli; 9 nami nimekuwa pamoja nawe kila ulikokwenda, na kuwakatilia mbali adui zako wote mbele yako; nami nitakufanyia jina kuu, kama jina la wakuu walioko duniani. 10 Tena nitawaagizia mahali watu wangu Israeli, nami nitawapanda, wapate kukaa mahali pao wenyewe, wasiondolewe tena; wala wana wa uovu hawatawatesa tena, kama hapo kwanza; 11 naam, kama vilivyokuwa tangu siku ile nilipowaamuru waamuzi, wawe juu ya watu wangu Israeli; nami nitakustarehesha mbele ya adui zako wote. Tena Bwana anakuambia ya kwamba Bwana atakujengea nyumba. 12 Nawe siku zako zitakapotimia, ukalala na baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayetoka viunoni mwako, nami nitaufanya imara ufalme wake. 13 Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele. 14 Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu; akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu; 15 lakini fadhili zangu hazitamwondoka, kama vile nilivyomwondolea Sauli, niliyemwondoa mbele yako. 16 Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele. 17 Kwa maneno hayo yote, na kwa maono hayo yote, ndivyo Nathani alivyonena na Daudi. 18 Ndipo Daudi, mfalme, akaingia, akaketi mbele za Bwana, akasema, Mimi ni nani, Bwana MUNGU, na nyumba yangu ni nini, hata umenileta hata hapa? 19 Tena jambo hili lilikuwa dogo machoni pako, Ee Bwana MUNGU; hata umeleta habari ya nyumba yangu mimi, mtumwa wako, kwa miaka mingi inayokuja baadaye; na hayo kwa namna ya kibinadamu, Ee Bwana MUNGU. 20 Na mimi, Daudi, nikuambie nini tena zaidi? Iwapo wewe umemjua mtumwa wako, Ee Bwana MUNGU. 21 Kwa ajili ya neno lako, na kwa moyo wako mwenyewe, umetenda makuu hayo yote, ili umjulishe mtumwa wako. 22 Kwa hiyo, wewe ndiwe mkuu, Ee Bwana Mungu, kwa maana hakuna kama wewe, wala hapana Mungu mwingine ila wewe, kwa kadiri tulivyosikia kwa masikio yetu. 23 Tena ni taifa lipi duniani lililo kama watu wako, kama Israeli, ambalo Mungu alikwenda kuwakomboa kwa ajili yake, wawe watu wake mwenyewe, akajifanyie jina, na kutenda mambo makuu kwa ajili yenu, na mambo ya kuogofya kwa ajili ya nchi yako, mbele ya watu wako, uliowakomboa kutoka Misri wawe wako, kutoka katika mataifa na miungu yao. 24 Nawe ulijifanyia imara watu wako Israeli, wawe watu wako milele; nawe, Bwana, umekuwa Mungu wao. 25 Basi sasa, Ee Bwana Mungu, neno lile ulilolinena katika habari za mtumwa wako, na katika habari za nyumba yangu, ulifanye imara milele, ukatende kama ulivyosema. 26 Jina lako na litukuzwe milele, kusema, Bwana wa majeshi ndiye Mungu juu ya Israeli; na nyumba ya mtumwa wako, Daudi, itakuwa imara mbele zako. 27 Kwa kuwa wewe, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli umenifunulia mimi, mtumwa wako, ukisema, Nitakujengea nyumba; kwa hiyo mimi, mtumwa wako, nimeona vema moyoni mwangu nikuombe dua hii. 28 Na sasa, Ee Bwana MUNGU, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ndiyo kweli, nawe umemwahidia mtumwa wako jambo hili jema 29 basi, sasa, uwe radhi, ukaibarikie nyumba ya mtumwa wako, ipate kudumu milele mbele zako; kwa maana wewe, Ee Bwana MUNGU, umelinena na kwa baraka yako nyumba ya mtumwa wako na ibarikiwe milele.

2 Samweli 8

1 Ikawa baadaye, Daudi akawapiga Wafilisti, akawashinda; Daudi akautwaa Gathi na vijiji vyake mikononi mwa hao Wafilisti. 2 Akapiga Moabu, akawapima kwa kamba hali wamelazwa chini; akapima kamba mbili za kuuawa, na kamba moja nzima ya kuhifadhi hai. Wamoabi wakawa watumwa wa Daudi, wakaleta zawadi. 3 Tena Daudi akampiga Hadadezeri mwana wa Rehobu, mfalme wa Soba, alipokwenda kujipatia tena mamlaka yake huko Mtoni. 4 Daudi akampokonya wapanda farasi elfu na mia saba na askari waliokwenda kwa miguu ishirini elfu; Daudi akawakata mshipa farasi wote wa magari, ila farasi wa magari mia akawasaza. 5 Na Washami wa Dameski walipokuja kumsaidia Hadadezeri, mfalme wa Soba, Daudi akawapiga wa Washami watu ishirini na mbili elfu. 6 Daudi akaweka ngome katika Shamu ya Dameski, na hao Washami wakawa watumwa wa Daudi, wakaleta zawadi. Naye Bwana akampa Daudi kushinda kila alikokwenda. 7 Tena Daudi akazitwaa ngao za dhahabu zilizovaliwa na watumwa wa Hadadezeri, akazileta Yerusalemu. 8 Tena toka Tebhathi na toka Berothai, miji ya Hadadezeri, Daudi akatwaa shaba nyingi mno. 9 Na Tou, mfalme wa Hamathi, aliposikia ya kwamba Daudi amewapiga jeshi lote la Hadadezeri, 10 Tou akamtuma kwa Daudi Hadoramu mwanawe kusalimia, na kumbarikia, kwa sababu amepigana na Hadadezeri, na kumpiga; kwa maana Hadadezeri alikuwa amepigana vita juu ya Tou. Na mkononi mwake akaleta vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na vyombo vya shaba; 11 hivi pia mfalme Daudi akavifanya wakfu kwa Bwana, pamoja na hiyo fedha, na dhahabu alizofanya wakfu za mataifa yote aliowashinda; 12 za Edomu, na za Moabu, na za wana wa Amoni, na za Wafilisti, na za Amaleki, na za nyara za Hadadezeri, mwana wa Rehobu, mfalme wa Soba. 13 Basi Daudi akajipatia jina, aliporudi kutoka kuwapiga Waedomi katika Bonde la Chumvi, watu kumi na nane elfu. 14 Akaweka askari wenye kulinda ngome katika Edomu; katikati ya Edomu yote akaweka ngome, na Waedomi wote wakawa watumwa wa Daudi. Naye Bwana akampa Daudi kushinda kila alikokwenda. 15 Daudi akatawala juu ya Israeli wote; naye Daudi akawafanyia hukumu na haki watu wake wote. 16 Huyo Yoabu, mwana wa Seruya alikuwa juu ya jeshi; na Yehoshafati, mwana wa Ahiludi, mwenye kuandika tarehe; 17 na Sadoki, mwana wa Ahitubu, na Ahimeleki, mwana wa Abiathari walikuwa makuhani; na Shausha mwandishi; 18 na Benaya, mwana wa Yehoyada, alikuwa juu ya Wakerethi na Wapelethi; nao wana wa Daudi wakawa makuhani.

2 Samweli 9

1 Kisha Daudi akasema, Je! Amesalia mtu mmoja katika nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema kwa ajili ya Yonathani? 2 Palikuwa na mtumishi mmoja wa nyumba ya Sauli, jina lake Siba, basi wakamwita aende kwa Daudi; na mfalme akamwuliza, Wewe ndiwe Siba? Naye akasema Mimi, mtumwa wako ndiye. 3 Mfalme akasema, Je! Hakuna hata sasa mtu ye yote wa nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema ya Mungu? Siba akamwambia mfalme, Yonathani anaye mwana hata sasa, aliye na kilema cha mguu. 4 Mfalme akamwambia, Yuko wapi? Siba akamwambia mfalme, Tazama, yumo katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. 5 Basi mfalme Daudi akatuma watu, akamwondoa katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. 6 Basi Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli akaenda kwa Daudi, akaanguka kifudifudi, akasujudu. Daudi akasema, Mefiboshethi! Naye akaitika, Mimi hapa, mtumwa wako! 7 Daudi akamwambia, Usiogope, maana bila shaka nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako, nami nitakurudishia mashamba yote ya Sauli, baba yako; nawe utakula chakula mezani pangu daima. 8 Akasujudu, akasema, Mimi mtumwa wako ni nini, hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi? 9 Ndipo mfalme akamwita Siba, mtumwa wa Sauli, akamwambia, Mali yote yaliyokuwa ya Sauli na ya nyumba yake nimempa mwana wa bwana wako. 10 Nawe utamlimia nchi hiyo, wewe, na wanao, na watumwa wako; nawe utamletea mwana wa bwana wako matunda yake, apate chakula ale; lakini Mefiboshethi, mwana wa bwana wako, atakula chakula mezani pangu sikuzote. Basi huyo Siba alikuwa na wana kumi na watano na watumwa ishirini. 11 Ndipo Siba akamwambia mfalme, Mimi, mtumwa wako, nitatenda hayo yote kama bwana wangu, mfalme, alivyoniamuru. Na kwa habari za Mefiboshethi, mfalme alisema, Atakula mezani pangu, kama mmojawapo wa wana wa mfalme. 12 Huyo Mefiboshethi alikuwa na mwana mdogo, jina lake akiitwa Mika. Na watu wote waliokaa nyumbani mwa Siba walikuwa watumwa wa Mefiboshethi. 13 Basi Mefiboshethi akakaa Yerusalemu; maana alikuwa akila chakula sikuzote mezani pa mfalme; naye alikuwa na kilema cha miguu yote miwili.

2 Samweli 10

1 Ikawa baadaye, mfalme wa wana wa Amori akafa, akamiliki Hanuni, mwanawe, mahali pake. 2 Naye Daudi akasema, Nitamtendea wema Hanuni, mwana wa Nahasi, kama babaye alivyonitendea wema mimi. Basi Daudi akatuma kwa mkono wa watumishi wake, ili kumtuliza kwa habari za babaye. Wakaja watumishi wa Daudi katika nchi ya wana wa Amoni. 3 Lakini wakuu wa wana wa Amoni wakamwambia Hanuni, bwana wao, Je! Waona ya kuwa Daudi amemheshimu babayo kwa kutuma kwako wafariji? Je! Daudi hakuwapeleka watumishi wake kwako ili kuuangalia mji, na kuupeleleza, na kuuangamiza? 4 Basi Hanuni akawatwaa hao watumishi wa Daudi, akawanyoa nusu ya ndevu zao, akawakatia nguo zao katikati, hata matakoni, akawatoa waende zao. 5 Watu walipomwambia Daudi habari hizo, akatuma watu kuwalaki; kwa sababu watu hao walikuwa wametahayarika sana. Mfalme akasema, Ngojeni Yeriko, hata mtakapoota ndevu zenu, ndipo mrudi. 6 Na wana wa Amoni walipoona ya kuwa wamekuwa machukizo kwa Daudi, wana wa Amoni wakatuma na kuwaajiri Washami wa Bethrehobu, na Washami wa Soba, askari ishirini elfu, na mfalme wa Maaka mwenye watu elfu, na watu wa Tobu watu kumi na mbili elfu. 7 Naye Daudi aliposikia akamtuma Yoabu, na jeshi lote la mashujaa. 8 Wana wa Amoni wakatoka, wakapanga vita mahali pa kuingilia lango; na Washami wa Soba, na wa Rehobu, na watu wa Tobu, na wa Maaka, walikuwa peke yao uwandani. 9 Basi Yoabu alipoona ya kwamba uso wa vita umekuwa juu yake mbele na nyuma, akachagua baadhi ya wateule wote wa Israeli, akawapanga juu ya Washami; 10 akawatia nguvu watu waliosalia mkononi mwa Abishai, nduguye, akawapanga juu ya wana wa Amoni. 11 Akasema, Wakiwa Washami hodari mno kwangu, ndipo wewe utanisaidia, lakini wana wa Amoni wakiwa ni hodari mno kwako, ndipo mimi nitakuja nikusaidie wewe. 12 Uwe hodari, tukajitie moyo mkuu, kwa ajili ya watu wetu, na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; naye Bwana afanye yaliyo mema machoni pake. 13 Basi Yoabu na watu waliokuwa pamoja naye wakakaribia kupigana na Washami; nao wakakimbia mbele yake. 14 Na wana wa Amoni walipoona ya kwamba Washami wamekimbia, wakakimbia nao mbele ya Abishai, wakaingia mjini. Ndipo Yoabu akarudi kutoka kwa wana wa Amoni, akaja Yerusalemu. 15 Na Washami walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, wakakusanyika. 16 Naye Hadadezeri akatuma na kuwaleta Washami waliokuwako ng'ambo ya Mto; nao wakaja Helamu, naye Shobaki, jemadari wa jeshi la Hadadezeri, akawaongoza. 17 Alipoambiwa Daudi, akakusanya Israeli wote, akavuka Yordani, akaja Helamu. Nao Washami wakajipanga kinyume cha Daudi, wakapigana naye. 18 Wakakimbia Washami mbele ya Israeli; naye Daudi akawaua katika Washami, watu wa magari mia saba, na wapanda farasi arobaini elfu, naye akampiga huyo Shobaki, jemadari wa jeshi lao, hata akafa huko. 19 Na wafalme wote waliomtumikia Hadadezeri walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, walifanya amani na Israeli, wakawatumikia. Basi Washami wakaogopa kuwasaidia wana wa Amoni tena.

2 Samweli 11

1 Hata ikawa, mwanzo wa mwaka mpya, wakati watokapo wafalme kwenda vitani, Daudi akampeleka Yoabu, na watumishi wake pamoja naye, na Israeli wote; wakawaangamiza wana wa Amoni, wakauhusuru Raba. Lakini Daudi mwenyewe akakaa Yerusalemu. 2 Ikawa wakati wa jioni, Daudi akaondoka kitandani, akatembea juu ya dari ya jumba la mfalme; na alipokuwa juu ya dari aliona mwanamke anaoga; naye huyo mwanamke alikuwa mzuri sana, wa kupendeza macho. 3 Naye Daudi akapeleka, akauliza habari za yule mwanamke. Mtu mmoja akasema, Je! Huyu siye Bath-sheba, binti Eliamu, mkewe Uria, Mhiti? 4 Basi Daudi akapeleka wajumbe, akamtwaa; naye akaingia kwake; naye akalala naye; (maana yule mwanamke amekwisha kutakasika unajisi wake); kisha akarudi nyumbani kwake. 5 Yule mwanamke akachukua mimba; basi akapeleka na kumwambia Daudi, akasema, Ni mja-mzito. 6 Ndipo Daudi akapeleka kwa Yoabu, akisema, Unipelekee Uria, Mhiti. Naye Yoabu akampeleka Uria kwa Daudi. 7 Uria alipomwendea Daudi, Daudi alimwuliza habari za Yoabu, na habari za watu, na habari za vita. 8 Daudi akamwambia Uria, Haya, shuka nyumbani kwako, ukanawe miguu yako. Basi Uria akatoka katika nyumba ya mfalme, na tunu ya vyakula ikamfuata, iliyotoka kwa mfalme. 9 Lakini Uria akalala mlangoni pa nyumba ya mfalme, pamoja na watumishi wote wa bwana wake, wala hakushuka nyumbani kwake. 10 Watu walipomwambia Daudi ya kwamba, Uria hakushuka nyumbani kwake, Daudi akamwambia Uria, Je! Hukutoka safarini? Mbona hukushuka nyumbani kwako? 11 Naye Uria akamwambia Daudi, Sanduku, na Israeli, na Yuda, wanakaa vibandani; na bwana wangu Yoabu, na watumishi wa bwana wangu, wamepiga kambi waziwazi uwandani; nami niende nyumbani kwangu, kula na kunywa, na kulala na mke wangu? Uishivyo, na kama roho yako iishivyo, mimi sitafanya jambo hili. 12 Basi Daudi akamwambia Uria, Ngoja hapa leo tena, na kesho nitakuacha kwenda zako. Basi Uria akakaa Yerusalemu siku ile, na siku ya pili yake. 13 Naye Daudi akamwalika, akala, akanywa mbele yake; naye akamlevya; hata wakati wa jioni akatoka kwenda kulala kitandani mwake pamoja na watumishi wa bwana wake, lakini hakushuka nyumbani kwake. 14 Hata ikawa asubuhi, Daudi akamwandikia Yoabu waraka, akaupeleka kwa mkono wa Uria. 15 Akaandika katika waraka huo, kusema, Mwekeni Uria mbele ya watu penye vita vikali, kisha ondokeni, mmwache, ili apigwe akafe. 16 Ikawa, Yoabu alipokuwa akiuhusuru mji, akamweka Uria mahali alipojua ya kuwa pana mashujaa. 17 Watu wa mji wakatoka, wakapigana na Yoabu; na baadhi ya watu, watumishi wa Daudi, wakaanguka; Uria Mhiti naye akafa. 18 Ndipo Yoabu akapeleka na kumwarifu Daudi habari zote za vita; 19 akamwagiza yule mjumbe, akisema, Ukiisha kumpa mfalme habari zote za vita, 20 itakuwa, hasira ya mfalme ikiwaka, akakuambia, Kwani mliukaribia mji namna ile ili kuupiga? Je! Hamkujua ya kuwa watapiga mishale toka ukutani? 21 Ni nani aliyempiga Ahimeleki, mwana wa Yeru-beshethi? Je! Si mwanamke aliyemtupia jiwe la kusagia la juu kutoka ukutani? Hata akafa huko Thebesi? Kwani kuukaribia ukuta namna ile? Ndipo utakaposema, Mtumishi wako Uria, Mhiti, amekufa naye. 22 Basi yule mjumbe akaenda, akafika na kumwonyesha Daudi yote aliyomtuma Yoabu. 23 Yule mjumbe akamwambia Daudi, Watu hao walitushinda, wakatutokea nje hata uwandani, tukashindana nao hata mahali pa kuingilia langoni. 24 Wapiga mishale wakatupiga sisi, watumishi wako, toka juu ya ukuta; na baadhi ya watumishi wa mfalme wamekufa, na Uria, Mhiti, mtumishi wako, amekufa naye. 25 Basi Daudi akamwambia yule mjumbe, Basi, mwambie Yoabu maneno haya, Jambo hili lisiwe baya machoni pako, maana upanga hula huyu kama unavyomla huyu; zidi kutia nguvu vita vyako juu ya mji ukauangushe; nawe mtie moyo. 26 Na yule mke wa Uria alipopata habari ya kuwa Uria mumewe amekufa, akamwombolezea mumewe. 27 Hata maombolezo hayo yalipokwisha, Daudi akatuma mtu, akamtwaa, akamtia nyumbani mwake; naye akawa mkewe, akamzalia mwana. Lakini jambo lile alilolitenda Daudi likamchukiza Bwana.

2 Samweli 12

1 Ndipo Bwana akamtuma Nathani aende kwa Daudi. Naye akamwendea, akamwambia, Palikuwa na watu wawili katika mji mmoja; mmoja wao alikuwa tajiri, wa pili maskini. 2 Yule tajiri alikuwa na kondoo na ng'ombe wengi sana; 3 bali yule maskini hakuwa na kitu, ila mwana kondoo mmoja, mdogo, ambaye amemnunua na kumlea; naye akakua pamoja naye, na pamoja na wanawe; hula sehemu ya posho lake, na kukinywea kikombe chake, na kulala kifuani mwake, akawa kwake kama binti. 4 Hata msafiri mmoja akamfikilia yule tajiri, naye akaacha kutwaa mmoja wa kondoo zake mwenyewe au mmoja wa ng'ombe zake mwenyewe, ili kumwandalia yule msafiri aliyemfikilia, bali alimnyang'anya yule maskini mwana-kondoo wake, akamwandalia yule mtu aliyemfikilia. 5 Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa; 6 naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma. 7 Basi Nathani akamwambia Daudi, Wewe ndiwe mtu huyo. Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nalikutia mafuta, uwe mfalme juu ya Israeli, nikakuokoa na mkono wa Sauli; 8 nami nikakupa nyumba ya bwana wako, na wake za bwana wako kifuani mwako; nikakupa nyumba ya Israeli na ya Yuda; na kama hayo yangalikuwa machache, ningalikuongezea mambo kadha wa kadha. 9 Kwa nini umelidharau neno la Bwana, na kufanya yaliyo mabaya machoni pake? Umempiga Uria, Mhiti, kwa upanga, nawe umemtwaa mkewe awe mke wako, nawe umemwua huyo kwa upanga wa wana wa Amoni. 10 Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako. 11 Bwana asema hivi, Angalia, nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, nami nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili. 12 Maana wewe ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua. 13 Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa. 14 Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa. 15 Naye Nathani akaondoka kwenda nyumbani kwake. Basi Bwana akampiga yule mtoto ambaye mkewe Uria alimzalia Daudi naye akawa hawezi sana. 16 Basi Daudi akamwomba Mungu kwa ajili ya mtoto; Daudi akafunga, akaingia, akalala usiku kucha chini. 17 Nao wazee wa nyumba yake wakaondoka, wakasimama karibu naye, ili wamwinue katika nchi; lakini hakukubali, wala hakula chakula pamoja nao. 18 Ikawa siku ya saba, yule mtoto akafa. Nao watumishi wa Daudi wakaogopa kumwambia ya kuwa mtoto amekufa, maana, walisema, Angalieni, yule mtoto alipokuwa angali hai, tulisema naye, asitusikilize sauti zetu; basi hatazidi kujisumbua, tukimwambia ya kuwa mtoto amekufa? 19 Lakini alipoona ya kuwa watumishi wake wananong'onezana, Daudi alitambua ya kuwa mtoto amekufa; basi Daudi akawauliza watumishi wake, Je! Mtoto amekufa? Nao wakasema, Amekufa. 20 Ndipo Daudi akainuka pale chini akaoga, akajipaka mafuta, akabadili mavazi yake; akaingia nyumbani mwa Bwana, akasali; kisha akaenda nyumbani kwake, na alipotaka wakamwandalia chakula, naye akala. 21 Watumishi wake wakamwambia, Ni neno gani hili ulilolitenda? Ulifunga na kulia kwa ajili ya mtoto, alipokuwa hai; lakini mtoto alipokuwa amekufa, uliinuka ukala chakula. 22 Akasema, Mtoto alipokuwa hai, nalifunga, nikalia; kwa maana nalisema, Ni nani ajuaye kwamba Bwana atanihurumia, mtoto apate kuishi? 23 Lakini sasa amekufa nifungie nini? Je! Naweza kumrudisha tena? Mimi nitakwenda kwake lakini yeye hatanirudia mimi. 24 Naye Daudi akamfariji Bath-sheba mkewe, akaingia kwake, akalala naye; naye akazaa mwana, akamwita jina lake Sulemani. Naye Bwana akampenda; 25 akapeleka kwa mkono wa Nathani, nabii, naye akamwita jina lake Yedidia, kwa ajili ya Bwana. 26 Yoabu akapigana juu ya Raba wa wana wa Amoni, akautwaa mji wa kifalme. 27 Yoabu akatuma wajumbe waende kwa Daudi, kusema Nimeshindana na Raba, hata nimeutwaa huo mji wa maji. 28 Basi sasa kusanya watu waliobaki, ukauzunguke mji, na kuutwaa; nisije mimi nikautwaa mji, ukaitwe jina langu. 29 Basi Daudi akawakusanya watu wote akaenda Raba, akapigana nao, akautwaa. 30 Kisha akamnyang'anya mfalme wao taji toka kichwani pake; na uzani wake ulikuwa talanta ya dhahabu, nayo ilikuwa na vito vya thamani ndani yake; akavikwa Daudi kichwani. Akazitoa nyara za huo mji, nyingi sana. 31 Naye akawatoa watu waliokuwamo, akawaweka kwenye kazi ya misumeno,na sululu za chuma,na mashoka ya chuma,akawatumikisha,tanuuni mwa matofali ndivyo alivyoifanya miji yote ya wana wa Amoni.Kisha Daudi akarudi na watu wote Yerusalemu.

2 Samweli 13

1 Ikawa baada ya hayo, Absalomu, mwana wa Daudi, alikuwa na umbu mzuri, jina lake akiitwa Tamari, naye Amnoni, mwana wa Daudi, akampenda. 2 Akasononeka Amnoni, hata akaugua, kwa ajili ya umbu lake Tamari, maana huyu msichana alikuwa mwanamwali, Amnoni akaona ni vigumu kumtendea neno lo lote. 3 Lakini Amnoni alikuwa na rafiki, jina lake Yonadabu, mwana wa Shama, nduguye Daudi; naye Yonadabu alikuwa mtu mwerevu sana. 4 Naye akamwambia, Kwa nini, Ee mwana wa mfalme, unakonda hivi siku kwa siku? Hutaki kuniambia? Amnoni akamwambia, Nampenda Tamari, umbu la ndugu yangu, Absalomu. 5 Yonadabu akamwambia, Lala kitandani mwako ujifanye mgonjwa na babako atakapokuja kukutazama, umwambie, Mwache ndugu yangu, Tamari, aje, nakusihi, anipe mkate nile, akaandae chakula machoni pangu nikione, nikakile mkononi mwake. 6 Basi Amnoni akalala, akajifanya mgonjwa; na mfalme alipokuja kumtazama, Amnoni akamwambia mfalme Mwache ndugu yangu, Tamari, aje, nakusihi, aniandalie mikate miwili machoni pangu, nipate kula mkononi mwake. 7 Basi Daudi akatuma mjumbe aende nyumbani kwa Tamari, akasema, Nenda sasa nyumbani kwa Amnoni, ndugu yako, ukamwandalie chakula. 8 Akaenda Tamari nyumbani kwa nduguye Amnoni; naye alikuwa amelala. Akachukua unga, akaukanda, akaiandaa mikate machoni pake, akaioka mikate. 9 Akalitwaa kaango, akaisongeza mbele yake; lakini alikataa kula. Naye Amnoni akasema, Toeni watu wote kwangu. Wakatoka kila mtu kwake. 10 Amnoni akamwambia Tamari, Kilete chakula chumbani, nipate kula mkononi mwako. Basi Tamari akaitwaa mikate aliyoifanyiza, akamletea Amnoni nduguye mle chumbani. 11 Naye alipokwisha kuileta karibu naye, ili ale, Amnoni akamkamata, akamwambia, Njoo ulale nami, ndugu yangu. 12 Naye akamjibu, La, sivyo, ndugu yangu, usinitenze nguvu; kwani haifai kutendeka hivi katika Israeli; usitende upumbavu huu. 13 Nami nichukue wapi aibu yangu? Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu wa Israeli. Basi, sasa, nakusihi, useme na mfalme; kwa maana hatakukataza kunioa. 14 Walakini yeye hakukubali kusikiliza sauti yake; naye akiwa na nguvu kuliko yeye, akamtenza nguvu, akalala naye. 15 Kisha Amnoni akamchukia machukio makuu sana; kwa kuwa machukio aliyomchukia yakawa makuu kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza. Amnoni akamwambia, Ondoka, nenda zako. 16 Naye akamwambia, Sivyo, kwa kuwa mabaya haya ya kunitoa ni makuu kuliko yale uliyonitendea. Lakini alikataa kumsikiliza. 17 Ndipo akamwita mtumishi wake aliyemtumikia, akasema, Mtoe sasa mwanamke huyu kwangu, ukafunge mlango nyuma yake. 18 Naye alikuwa amevaa kanzu ndefu; kwa kuwa kwa nguo hizo huvikwa binti za mfalme waliokuwa wanawali. Ndipo mtumishi wake akamleta nje, akafunga mlango nyuma yake. 19 Naye Tamari akatia majivu kichwani mwake, akairarua hiyo kanzu ndefu yake aliyoivaa, akaweka mkono kichwani akaenda zake huku akilia kwa sauti. 20 Huyo Absalomu nduguye akamwambia, je! Amekuwa nawe Amnoni nduguyo? Ila sasa tulia, dada; ni nduguyo; usilitie moyoni jambo hili. Basi Tamari akakaa hali ya ukiwa nyumbani mwa nduguye Absalomu. 21 Na mfalme Daudi alipoyasikia maneno hayo yote, alikasirika sana. 22 Ila Absalomu hakusema na Amnoni wala kwa heri wala kwa shari; kwa maana Absalomu alimchukia Amnoni kwa kumtenza nguvu umbu lake Tamari. 23 Ikawa baada ya miaka miwili mizima, Absalomu alikuwa na wenye kukata manyoya ya kondoo huko Baal-hasori uliopo upande wa Efraimu; naye Absalomu akawaalika wana wote wa mfalme. 24 Absalomu akamjia mfalme, akasema, Tazama sasa, mimi mtumwa wako ninao wakata manyoya ya kondoo; basi mfalme na aende, nakusihi, na watumishi wake pamoja nami mtumwa wako. 25 Mfalme akamwambia Absalomu, Sivyo, mwanangu, tusiende sote, tusije tukakulemea. Akamsihi sana; asikubali kwenda, ila akambariki. 26 Ndipo akasema Absalomu, Kwamba huji, nakusihi, mwache ndugu yangu Amnoni aende nasi. 27 Mfalme akamwambia, Kwa nini aende nawe? Lakini Absalomu akamsihi sana, naye akamwacha Amnoni na wana wote wa mfalme waende naye. 28 Kisha Absalomu akawaamuru watumishi wake, akasema, Angalieni basi, moyo wake Amnoni utakapofurahiwa kwa mvinyo; nami nitakapowaambia, Mpigeni Amnoni, ndipo mwueni, msiogope; si mimi niliyewaamuru? Iweni hodari, iweni na ujasiri. 29 Basi watumishi wa Absalomu wakamfanyia Amnoni kama alivyoamuru Absalomu. Ndipo wakaondoka wana wote wa mfalme, wakapanda kila mtu nyumbu wake, wakakimbia. 30 Ikawa, walipokuwa njiani, habari zikamwasilia Daudi, kusema, Absalomu amewaua wana wote wa mfalme, wala hata mmoja wao hakusalia. 31 Ndipo mfalme akainuka, akararua nguo zake, akalala chini; nao watumishi wake wote wakasimama karibu naye, wenye nguo zao zimeraruliwa. 32 Akajibu Yonadabu, mwana wa Shama, nduguye Daudi, akasema, Asidhani bwana wangu ya kwamba wamewaua vijana wote, wana wa mfalme; maana ndiye Amnoni peke yake aliyekufa; yakini haya yamekusudiwa kwa kinywa chake Absalomu tangu siku ile alipotenzwa nguvu umbu lake, Tamari. 33 Basi sasa bwana wangu mfalme asilitie neno hili moyoni, kudhani ya kwamba wana wote wa mfalme wamekufa maana ni Amnoni peke yake aliyekufa. 34 Lakini Absalomu akakimbia. Na kijana yule aliyekuwa mlinzi akainua macho yake, akaona, na tazama, kuna watu wengi wanakuja kwa njia ya upande wa kilima nyuma yake. 35 Ndipo Yonadabu akamwambia mfalme, Tazama, wana wa mfalme wamekuja; kama mimi mtumwa wako nilivyosema, ndivyo ilivyo. 36 Ikawa alipokwisha kusema, tazama, wana wa mfalme walikuja, nao wakapaza sauti zao wakalia; mfalme naye akalia, na watumishi wake wote, kilio kikubwa mno. 37 Lakini Absalomu akakimbia, akamwendea Talmai, mwana wa Amihuri, mfalme wa Geshuri. Naye Daudi akamlilia mwanawe kila siku. 38 Basi Absalomu akakimbia, akaenda Geshuri, akakaa huko muda wa miaka mitatu. 39 Mfalme Daudi akatamani kutoka kumwendea Absalomu kwa kuwa ametulizwa kwa habari ya Amnoni, kwa maana amekufa.

2 Samweli 14

1 Basi Yoabu, mwana wa Seruya, akatambua ya kuwa moyo wa mfalme unamwelekea Absalomu. 2 Yoabu akatuma watu waende Tekoa, akaleta kutoka huko mwanamke mwenye akili, akamwambia, Nakusihi, ujifanye kama unakaa matanga, ukavae nguo za kufiwa, nakusihi, wala usijitie mafuta, ila ukafanane na mwanamke aliyeomboleza siku nyingi kwa ajili yake aliyefariki; 3 kisha uingie kwa mfalme ukamwambie maneno haya. Hivyo Yoabu akamtia maneno kinywani. 4 Naye yule mwanamke wa Tekoa aliponena na mfalme, akaanguka kifulifuli chini, akamsujudia, akasema, Nisaidie, Ee mfalme. 5 Mfalme akamwuliza, Una nini? Naye akajibu, Hakika ni mjane mimi, niliyefiwa na mume wangu. 6 Nami mjakazi wako nalikuwa na wana wawili, na hao wawili wakashindana uwandani, wala hapakuwa na mtu wa kuwaamua, lakini mmoja akampiga mwenzake, akamwua. 7 Na tazama, jamaa yote wameniinukia mimi mjakazi wako, wakasema, Mtoe yule aliyempiga nduguye, ili tupate kumwua yeye kwa maisha ya nduguye aliyemwua, hata na kumfisha mrithi pia; ndivyo watakavyolizima kaa langu lililobaki, wasimwachie mume wangu jina wala masalio usoni pa nchi. 8 Mfalme akamwambia huyo mwanamke, Nenda nyumbani kwako, nami nitakufanyia agizo. 9 Ndipo huyo mwanamke wa Tekoa akamwambia mfalme, Na uwe juu yangu, Ee bwana wangu mfalme, na juu ya nyumba ya baba yangu uovu huu; wala kwa mfalme na kwa kiti chake cha enzi pasiwepo hatia. 10 Mfalme akasema, Ye yote atakaye kuambia neno, mlete kwangu, naye hatakugusa tena. 11 Ndipo akajibu, Nakusihi, mfalme na amkumbuke Bwana, Mungu wako, ili mlipiza kisasi cha damu asizidi kuharibu, wasije kumharibu mwanangu. Naye akasema, Aishivyo Bwana, hautaanguka chini hata unywele mmoja wa mwanao. 12 Mwanamke akasema, Mwache mjakazi wako, nakusihi, niseme neno moja kwa bwana wangu mfalme. Akasema, Haya nena. 13 Mwanamke akasema, Kwa nini basi wewe umewafikiria mambo kama hayo watu wa Mungu? Kwani kwa kunena neno hili mfalme ni kama mwenye hatia, kwa kuwa mfalme hamleti kwao tena yule mfukuzwa wake. 14 Kwa kuwa hatuna budi kufa, nasi tu kama maji yaliyomwagika chini, yasiyowezekana kuzoleka tena; wala Mungu haondoi maisha ila hufikiri shauri, kwamba yeye aliyefukuzwa asiwe mkimbizi kwake. 15 Hata sasa nilivyokuja mimi kunena neno hili na bwana wangu mfalme, ni kwa sababu watu wamenitisha; nami, mjakazi wako, nikasema, Mimi nitanena sasa kwa mfalme; labda itakuwa mfalme atanifanyia haja yangu mimi mtumwa wake. 16 Kwa kuwa mfalme atasikia, ili amwokoe mtumwa wake mkononi mwa yule mtu atakaye kuniharibu mimi na mwanangu pia katika urithi wa Mungu. 17 Ndipo mimi mjakazi wako nikasema, Neno la bwana wangu mfalme na liwe la kustarehesha; kwa kuwa kama malaika wa Mungu ndivyo alivyo bwana wangu mfalme, kuyapambanua yaliyo mema na yaliyo mabaya; naye Bwana, Mungu wako na awe pamoja nawe. 18 Ndipo mfalme akajibu, akamwambia yule mwanamke, usinifiche, nakusihi, neno lo lote nitakalokuuliza. Na mwanamke akasema, Na anene sasa bwana wangu mfalme. 19 Mfalme akasema, Je! Si mkono wa Yoabu ulio pamoja nawe katika haya yote? Mwanamke akajibu, akasema, Kama iishivyo roho yako, bwana wangu, mfalme, hapana mtu awezaye kugeuka kwa kuume, au kwa kushoto, kukana neno lo lote alilolisema bwana wangu mfalme; kwani mtumwa wako Yoabu ndiye aliyeniamuru, na kuyaweka maneno haya yote kinywani mwa mjakazi wako; 20 mtumwa wako Yoabu ameyatenda haya ili kubadili uso wa jambo hili; na bwana wangu anayo akili, kama akili ya malaika wa Mungu, hata ajue mambo yote ya duniani. 21 Basi mfalme akamwambia Yoabu, Angalia sasa, nimekata shauri hili; nenda, ukamrudishe tena yule kijana Absalomu. 22 Naye Yoabu akaanguka kifulifuli hata nchi, akasujudu, akambariki mfalme, Yoabu akasema, Leo mimi mtumwa wako najua ya kwamba nimepata neema machoni pako, bwana wangu mfalme, kwa kuwa mfalme amemfanyia mtumwa wake haja yake. 23 Basi Yoabu akaondoka, akaenda Geshuri, akamleta Absalomu Yerusalemu. 24 Naye mfalme akasema, Ageukie nyumbani kwake, asinione uso wangu. Basi Absalomu akarejea nyumbani kwake, asimwone uso mfalme. 25 Basi katika Israeli wote hapakuwa na mtu hata mmoja mwenye kusifiwa kwa uzuri wake kama huyo Absalomu; tangu nyayo za miguu yake hata utosi wa kichwa chake hapakuwa na ila kwake. 26 Naye aliponyoa kichwa, (basi mwisho wa kila mwaka hunyoa; na kwa sababu nywele zilikuwa nzito kwake, kwa hiyo akanyoa;) hupima nywele za kichwa chake shekeli mia mbili kwa uzani wa mfalme. 27 Kisha wakazaliwa kwake Absalomu wana watatu na binti mmoja, ambaye jina lake aliitwa Tamari; naye alikuwa mwanamke mzuri wa uso. 28 Absalomu akakaa miaka miwili mizima katika Yerusalemu; asimwone uso mfalme. 29 Ndipo Absalomu akatuma kumwita Yoabu, ampeleke kwa mfalme, lakini yeye akakataa kumjia; akatuma tena mara ya pili, lakini akakataa kuja. 30 Kwa hiyo akawaambia watumishi wake, Tazameni, shamba la Yoabu liko karibu na shamba langu, naye ana shayiri huko; nendeni mkalitie moto. Basi watumishi wa Absalomu wakalitia moto lile shamba. 31 Ndipo akaondoka Yoabu, akamwendea Absalomu nyumbani kwake, akamwambia, Kwa nini watumishi wako wamelitia moto shamba langu? 32 Absalomu akamjibu Yoabu, Angalia, nilituma kwako, kusema, Njoo kwangu, ili nikupeleke kwa mfalme kunena, Mbona nimekuja kutoka Geshuri? Ingekuwa heri kwangu kama ningekuwako huko hata sasa; basi sasa na nimtazame uso mfalme; na ukiwapo uovu kwangu, na aniue. 33 Basi Yoabu akamwendea mfalme, akamwambia hayo, naye alipomwita Absalomu, yeye akaja kwa mfalme, akainama kifulifuli hata nchi mbele ya mfalme; naye mfalme akambusu Absalomu.

2 Samweli 15

1 Ikawa baada ya hayo, Absalomu akajiwekea tayari gari na farasi, na watu hamsini wa kupiga mbio mbele yake. 2 Tena Absalomu huondoka asubuhi na mapema, na kusimama kando ya njia ya lango; kisha ikawa, mtu ye yote aliyekuwa na neno, lililokuwa halina budi kufika kwa mfalme ili kuhukumiwa, Absalomu humwita mtu huyo kwake, na kumwuliza, Wewe u mtu wa mji gani? Naye akasema, Mtumwa wako ni mtu wa kabila fulani ya Israeli. 3 Naye Absalomu humwambia, Tazama, maneno yako ni mema yenye haki; lakini hapana mtu aliyeagizwa na mfalme kukusikiliza. 4 Tena Absalomu husema, Laiti mimi ningewekwa kuwa mwamuzi katika nchi hii, ili kila mtu mwenye neno au daawa aje kwangu, nimpatie haki yake! 5 Tena ikawa hapo alipokaribia mtu ye yote kumsujudia, hunyosha mkono wake, na kumshika, na kumbusu. 6 Hivyo ndivyo Absalomu alivyowatendea Israeli wote, waliomwendea mfalme ili wapate hukumu; na hivyo Absalomu akawadanganya watu wa Israeli. 7 Hata ikawa mwisho wa miaka minne, Absalomu akamwambia mfalme Tafadhali uniache niende nikaondoe nadhiri yangu, niliyomwekea Bwana huko Hebroni. 8 Maana mimi mtumishi wako naliweka nadhiri hapo nilipokuwa nikikaa Geshuri katika Shamu, nikasema, Kama Bwana akinirudisha Yerusalemu kweli, ndipo nitamtumikia Bwana. 9 Naye mfalme akamwambia, Enenda na amani. Basi akaondoka, akaenda Hebroni. 10 Lakini Absalomu akapeleka wapelelezi katika kabila zote za Israeli kusema, Mara mtakaposikia sauti ya tarumbeta, ndipo mtakaposema Absalomu anamilikl huko Hebroni. 11 Na watu mia mbili walioalikwa wakatoka Yerusalemu pamoja na Absalomu, wakaenda katika ujinga wao wasijue neno lo lote. 12 Absalomu naye akatuma kumwita Ahithofeli Mgiloni, mshauri wake Daudi, kutoka katika mji wake, yaani, Gilo, alipokuwa akitoa dhabihu. Fitina yao ikawa na nguvu; maana watu waliokuwa pamoja na Absalomu wakazidi kuwa wengi. 13 Mjumbe akamfikilia Daudi, akasema, Mioyo ya watu wa Israeli inashikamana na Absalomu. 14 Basi Daudi akawaambia watumishi wake wote waliokuwa pamoja naye Yerusalemu, Ondokeni, tukakimbie kwa kuwa tusipokimbia hapana mtu miongoni mwetu atakayeokoka mikononi mwa Absalomu; haya! Fanyeni haraka, tuondoke, asitupate kwa upesi, na kutuletea maovu, na kuupiga mji huu kwa makali ya upanga. 15 Hao watumishi wa mfalme wakamwambia mfalme, Angalia, sisi watumishi wako tu tayari kutenda lo lote atakalolichagua bwana wetu mfalme. 16 Basi mfalme akatoka na watu wa nyumbani mwake wote wakafuatana naye. Mfalme akaacha wanawake kumi, masuria, ili kuitunza nyumba. 17 Mfalme akatoka, na watu wote wakamfuata; wakakaa kidogo katika Beth-merhaki. 18 Watumishi wake wote wakapita karibu naye; na Wakerethi wote, na Wapelethi wote, na Wagiti wote, watu mia sita walioandamana naye kutoka Gathi, wakapita mbele ya mfalme. 19 Ndipo mfalme akamwambia Itai, Mgiti, Mbona wewe unakwenda pamoja nasi? Rudi, ukakae na mfalme; maana wewe u mgeni, tena u mtu uliyefukuzwa mahali pako mwenyewe. 20 Kwa kuwa umekuja jana tu kwa nini nikusumbue leo, na kukuzungusha huko na huko pamoja nasi nami hapa naenda niwezapo kwenda? Rudi wewe, ukawarudishe na ndugu zako; rehema na kweli ziwe pamoja nawe. 21 Naye Itai akamjibu mfalme akasema, Kama aishivyo Bwana, na bwana wangu mfalme aishivyo, hakika yake kila mahali atakapokuwapo mfalme, bwana wangu, ikiwa ni kwa kufa au ikiwa ni kwa kuishi, ndipo atakapokuwapo na mtumwa wako. 22 Basi Daudi akamwambia Itai, Haya, enenda ukavuke. Akavuka Itai, Mgiti na watu wake wote, na watoto wadogo wote waliokuwa pamoja naye. 23 Na nchi yote ikalia kwa sauti kuu, nao watu wote wakavuka, mfalme mwenyewe naye akavuka kile kijito Kidroni, na hao watu wote wakavuka, wakielekea njia ya nyika. 24 Na tazama, Sadoki naye akaja, na Walawi wote pamoja naye, huku wakilichukua sanduku la agano la Mungu; kisha wakalitua hilo sanduku la Mungu; Abiathari naye akapanda juu, hata watu wote walipokwisha kuutoka mji. 25 Naye mfalme akamwambia Sadoki, Rudisha sanduku la Mungu mjini; nikipata kibali machoni pa Bwana atanirudisha, na kunionyesha tena sanduku hili, na maskani yake; 26 lakini akisema kama hivi, Mimi si radhi nawe kabisa; basi, mimi hapa, na anitendee kama aonavyo kuwa vyema. 27 Kisha mfalme akamwambia Sadoki, kuhani, Angalia, rudini mjini kwa amani, na wana wenu wawili pamoja nanyi,Ahimaasi,mwana wako, na Yonathani,mwana wa Abiathari. 28 Angalia, mimi nitangoja penye vivuko vya jangwani, hata litakaponifikilia neno la kunipasha habari kutoka kwenu. 29 Basi Sadoki na Abiathari wakalichukua sanduku la Mungu, wakalirudisha Yerusalemu; wakakaa huko. 30 Daudi akapanda akishika njia ya kuupandia mlima wa Mizeituni, akilia alipokuwa akipanda; naye alikuwa amejifunika kichwa chake, akaenda hana viatu; na watu wote waliokuwa pamoja naye wakajifunika vichwa vyao, kila mmoja wao, wakapanda juu, wakilia walipopanda. 31 Mtu mmoja akamwambia Daudi ya kwamba, Ahithofeli yu katika hao waliopatana na Absalomu; Daudi akasema, Ee Bwana, nakusihi, uligeuze shauri la Ahithofeli liwe ubatili. 32 Ikawa, Daudi alipofika juu, hapo Mungu alipoabudiwa, tazama, Hushai, Mwarki, akaja kumlaki na joho lake limeraruliwa, tena ana udongo kichwani mwake. 33 Daudi akamwambia, Ukienda mbele pamoja nami, utakuwa mzigo kwangu; 34 lakini ukirudi mjini, na kumwambia Absalomu, Nitakuwa mtumishi wako, Ee mfalme; kama vile nilivyokuwa mtumishi wa baba yako tokea zamani, ndivyo nitakavyokuwa mtumishi wako sasa; ndipo utayavunja mashauri ya Ahithofeli kwa ajili yangu. 35 Je! Hawako Sadoki na Abiathari, makuhani, pamoja nawe huko? Basi itakuwa, kila neno utakalolisikia katika jumba la mfalme, utawaambia Sadoki na Abiathari, makuhani. 36 Angalia, wanao huko pamoja nao wana wao wawili, Ahimaasi, mwana wa Sadoki, na Yonathani, mwana wa Abiathari; nanyi kwa mikono yao mtanipelekea habari ya kila neno mtakalolisikia. 37 Basi Hushai, rafiki wa Daudi, akaingia ndani ya mji; naye Absalomu akafika akaingia Yerusalemu.

2 Samweli 16

1 Naye Daudi alipokipita punde hicho kilele cha mlima, tazama, Siba, mtumwa wa Mefiboshethi, akamkuta, na punda wawili waliotandikwa, na juu yao mikate mia mbili ya ngano, na vishada mia vya zabibu kavu, na matunda mia ya wakati wa hari, na kiriba cha divai. 2 Mfalme akamwambia Siba, Ni za nini hizi? Siba akasema, Punda ni za jamaa ya mfalme wazipande; na mkate na matunda ni chakula cha hawa vijana; na divai ni kwamba wanywe hao wazimiao nyikani. 3 Mfalme akasema, Na mwana wa bwana wako yuko wapi? Siba akamwambia mfalme, Angalia, anakaa Yerusalemu; kwani alisema, Leo nyumba ya Israeli watanirudishia ufalme wa baba yangu. 4 Ndipo mfalme akamwambia Siba, Tazama, yote yaliyokuwa ni mali ya Mefiboshethi ni yako. Siba akasema, Mimi nasujudu; na nione kibali machoni pako, Ee bwana wangu, mfalme. 5 Basi mfalme Daudi alipofika Bahurimu, tazama, kulitoka huko mtu wa jamaa ya nyumba ya Sauli, jina lake akiitwa Shimei, mwana wa Gera; alitoka, akalaani alipokuwa akienda. 6 Tena akamtupia Daudi mawe, na watumishi wote wa mfalme Daudi; na watu wote na mashujaa wote walikuwako mkono wake wa kuume na mkono wake wa kushoto. 7 Na Shimei alipolaani, alisema hivi, Nenda zako! Nenda zako! Ewe mtu wa damu! Ewe mtu usiyefaa! 8 Bwana amerudisha juu yako damu yote ya nyumba ya Sauli ambaye umetawala badala yake; naye Bwana ametia ufalme katika mkono wa Absalomu mwanao; kisha, angalia, wewe umetwaliwa katika uovu wako mwenyewe, kwa sababu umekuwa mtu wa damu. 9 Ndipo Abishai mwana wa Seruya, akamwambia mfalme, Mbona mbwa mfu huyu amlaani mfalme bwana wangu? Na nivuke, nakusihi, nikaondoe kichwa chake. 10 Mfalme akasema, Nina nini na ninyi, enyi wana wa Seruya? Kwa sababu yeye analaani, na kwa sababu Bwana amemwambia, Mlaani Daudi, basi, ni nani atakayesema, Mbona umetenda haya? 11 Daudi akamwambia Abishai, na watumishi wake wote, Angalieni, huyu mwanangu, aliyetoka viunoni mwangu, anautafuta uhai wangu; si zaidi Mbenyamini huyu sasa? Mwacheni alaani, kwa sababu Bwana ndiye aliyemwagiza. 12 Labda Bwana atayaangalia mabaya yaliyonipata, naye Bwana atanilipa mema kwa sababu ya kunilaani kwake leo. 13 Basi wakaendelea njiani Daudi na watu wake; Shimei naye akaaendelea juu ya ubavu wa kile kilima, kwa kumkabili, huku akiendelea, akilaani, akimtupia mawe, na kurusha mavumbi. 14 Naye mfalme na watu wake wote waliokuwa pamoja naye wakafika, wamechoka sana; naye akajiburudisha huko. 15 Absalomu, na hao watu wote wa Israeli, wakafika Yerusalemu, naye Ahithofeli alikuwa pamoja naye. 16 Ikawa, Hushai, Mwarki, rafiki wa Daudi, alipomjia Absalomu, Hushai akamwambia Absalomu, Na aishi mfalme, aishi mfalme. 17 Naye Absalomu akamwambia Hushai, Je! Huu ndio wema wako kwa rafiki yako? Mbona hukutoka pamoja na rafiki yako? 18 Hushai akamwambia Absalomu, La, sivyo; lakini yule Bwana aliyemchagua, na watu hawa, na watu wote wa Israeli, mimi nitakuwa wake, na pamoja naye nitakaa. 19 Na tena, Ni nani ambaye yanipasa nimtumikie? Hainipasi kutumika mbele ya mwanawe? Kama nilivyotumika mbele ya baba yako, ndivyo nitakavyokuwa mbele yako. 20 Kisha Absalomu akamwambia Ahithofeli, Haya, toa shauri lako, tufanyeje. 21 Naye Ahithofeli akamwambia Absalomu, Ingia wewe kwa masuria ya baba yako, hao aliowaacha ili kutunza nyumba; na Israeli wote watasikia ya kuwa umechukizwa kabisa na baba yako; ndipo itatiwa nguvu mikono yao wote walio pamoja nawe. 22 Basi wakamtandikia Absalomu hema juu ya nyumba darini; naye Absalomu akaingia kwa masuria ya babaye machoni pa Israeli wote. 23 Na shauri lake Ahithofeli, alilokuwa akilitoa siku zile, lilikuwa kama mtu aulizapo kwa neno la Mungu; ndivyo yalivyokuwa mashauri yote ya Ahithofeli, kwa Daudi, na kwa Absalomu.

2 Samweli 17

1 Zaidi ya hayo Ahithofeli akamwambia Absalomu, Niache nichague watu kumi na mbili elfu, nami nitaondoka na kumfuatia Daudi usiku huu; 2 nami nitamshambulia wakati atakaokuwa amechoka, na mikono yake imekuwa dhaifu, nami nitamtia hofu; na watu wote walio pamoja naye watakimbia; nami nitampiga mfalme peke yake; 3 na hao watu wote nitawarejeza kwako; mtu yule umtafutaye ni kana kwamba wamerudi wote; na hivyo watu wote watakuwa katika amani. 4 Shauri hili likawa jema machoni pa Absalomu, na machoni pa wazee wote wa Israeli. 5 Ndipo Absalomu akasema, Basi, mwiteni Hushai, Mwarki, naye, tukasikie atakayosema yeye pia. 6 Basi Hushai alipofika kwa Absalomu, Absalomu akamwambia, akasema, Ahithofeli amesema hivi; je! Tufanye kama alivyosema? Kama sivyo, sema maneno yako. 7 Hushai akamwambia Absalomu, Shauri hili alilolitoa Ahithofeli si jema wakati huu. 8 Hushai akafuliza kusema, Wamjua baba yako na watu wake, ya kuwa ni watu mashujaa hawa, nao wana uchungu katika mioyo yao, kama dubu aliyenyang'anywa watoto wake nyikani; tena baba yako ni mtu wa vita, hatalala pamoja na watu wake. 9 Angalia, amefichwa sasa katika shimo, au penginepo; kisha itakuwa, watakapoanguka baadhi yao mwanzo, kila mtu atakayesikia, atasema, Kuna machinjo katika watu wanaofuatana na Absalomu. 10 Basi hata yeye aliye shujaa, mwenye moyo kama moyo wa simba, atayeyuka kabisa; maana Israeli wote wanajua ya kuwa baba yako ni shujaa, na ya kuwa watu wale walio pamoja naye ni mashujaa. 11 Kwa hiyo shauri langu ni hili, Waisraeli wote toka Dani mpaka Beer-sheba wakusanyike kwako, kama mchanga wa bahari kwa wingi; na wewe uende vitani mwenyewe. 12 Hivyo tutamfikia mahali po pote atakapoonekana, na kumwangukia kama vile umande uangukavyo juu ya nchi; wala hatutaacha hata mmoja wao, yeye na watu wote walio pamoja naye. 13 Tena, ikiwa amejitia katika mji uwao wote, basi Israeli wote wataleta kamba, na kuuendea mji ule, nasi tutaukokota mpaka mtoni, wala halitaonekana huko hata jiwe dogo moja la mawe yake. 14 Naye Absalomu na watu wote wa Israeli wakasema, Shauri la Hushai, Mwarki, ni jema kuliko shauri la Ahithofeli. Kwa maana Bwana alikuwa amekusudia kulivunja shauri jema la Ahithofeli, ili Bwana alete mabaya juu ya Absalomu. 15 Ndipo Hushai akawaambia Sadoki na Abiathari, makuhani, Ahithofeli amempa Absalomu na wazee wa Israeli mashauri kadha wa kadha; na mimi nimetoa mashauri kadha wa kadha. 16 Basi sasa pelekeni habari upesi kamwambieni Daudi ya kwamba, Usilale usiku huu karibu na vivuko vya jangwani; bali usikose kuvuka; asije akamezwa mfalme, na watu wote walio pamoja naye. 17 Basi Yonathani na Ahimaasi walikuwa wakikaa karibu na Enrogeli; na mjakazi mmoja alikuwa akienda na kuwapa habari; nao huenda kumwambia mfalme Daudi; maana ilikuwa lazima wasionekane wakiingia mjini. 18 Lakini kijana mmoja aliwaona, akamwambia Absalomu; basi wakaenda wote wawili kwa haraka, wakafika Bahurimu, nyumbani kwa mtu aliyekuwa na kisima uani mwake; wakashuka ndani yake. 19 Na mwanamke akatwaa kifuniko akakiweka juu ya mdomo wa kile kisima, akaanika ngano iliyotwangwa juu yake; wala halikujulikana neno lo lote. 20 Nao watumishi wa Absalomu wakamwendea yule mwanamke mle nyumbani; wakasema, Wako wapi Yonathani na Ahimaasi? Yule mwanamke akawaambia, Wamevuka kijito cha maji. Basi walipokwisha kuwatafuta wasiwaone, wakarudi Yerusalemu. 21 Kisha ikawa, baada ya kuondoka kwao, wale wakatoka kisimani, wakaenda wakamwarifu mfalme Daudi; wakamwambia Daudi, Ondokeni, mkavuke maji haya upesi; maana ndivyo alivyotoa shauri Ahithofeli juu yenu. 22 Ndipo Daudi, na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakaondoka, wakavuka Yordani; na kulipopambazuka hakubaki mmojawapo wao asiyevuka Yordani. 23 Naye Ahithofeli alipoona ya kuwa shauri lake halikufuatwa, akatandika punda wake, akaondoka, akaenda nyumbani kwake, mjini mwake, akaitengeneza nyumba yake, akajisonga; akafa, akazikwa kaburini mwa babaye. 24 Basi Daudi akaja Mahanaimu. Naye Absalomu akauvuka Yordani yeye na watu wote wa Israeli pamoja naye. 25 Naye Absalomu akamweka Amasa awe juu ya jeshi mahali pa Yoabu. Basi huyo Amasa alikuwa mwana wa mtu, jina lake Yetheri, Mwishmaeli, aliyeingia kwa Abigali, binti Nahashi, nduguye Seruya, mamaye Yoabu. 26 Israeli na Absalomu wakapiga kambi katika nchi ya Gileadi. 27 Ikawa, Daudi alipofika Mahanaimu, Shobi, mwana wa Nahashi wa Raba, wa wana wa Amoni, na Makiri, mwana wa Amieli wa Lo-debari, na Barzilai, Mgileadi wa Rogelimu, 28 wakaleta magodoro, na mabakuli, na vyungu, na ngano, na shayiri, na unga, na bisi, na kunde, na dengu, 29 na asali, na siagi, na kondoo, na samli ya ng'ombe, wapate kula Daudi na watu waliokuwa pamoja naye; kwani walisema, Watu hao waona njaa, tena wamechoka, nao wana kiu huku nyikani.

2 Samweli 18

1 Kisha Daudi akawahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akaweka maakida wa elfu elfu, na maakida wa mia mia juu yao. 2 Daudi akawapeleka hao watu vitani, theluthi moja chini ya mkono wa Yoabu, na theluthi ya pili chini ya mkono wa Abishai, mwana wa Seruya nduguye Yoabu, na theluthi ya tatu chini ya mkono wa Itai, Mgiti. Mfalme akawaambia watu, Bila shaka mimi mwenyewe nami nitatoka pamoja nanyi. 3 Lakini watu wakasema, Wewe usitoke nje; kwa maana tukikimbia, hawatatuona sisi kuwa kitu; au tukifa nusu yetu, hawatatuona kuwa kitu; lakini wewe u wa thamani kuliko watu elfu kumi katika sisi; kwa hivyo sasa ni afadhali ukae tayari kutusaidia toka mjini. 4 Mfalme akawaambia, Yaliyo mema machoni penu ndiyo nitakayofanya. Basi mfalme akasimama kando ya lango, na hao watu wakatoka kwa elfu zao na mia zao. 5 Mfalme akawaamuru Yoabu na Abishai na Itai, akasema, Mtendeeni yule kijana, Absalomu, kwa upole kwa ajili yangu. Nao watu wote wakasikia, mfalme alipowaagiza maakida wote katika habari za Absalomu. 6 Hivyo watu wakatoka waende nyikani ili kupigana na Israeli; na vita vikatokea ndani ya msitu wa Efraimu. 7 Watu wa Israeli wakapigwa huko mbele ya watumishi wa Daudi, kukawa na maangamizo makuu huko siku ile, ya watu ishirini elfu. 8 Kwa maana vita vilienea huko juu ya uso wote wa nchi; na siku ile huo msitu ukala watu wengi kuliko wale walioliwa na upanga. 9 Na kwa bahati Absalomu akakutana na watumishi wa Daudi. Naye Absalomu alikuwa amepanda nyumbu wake, na yule nyumbu akapita chini ya matawi manene ya mwaloni mkubwa, hata kichwa chake kikakwama katika mwaloni huo, akanyakuliwa juu kati ya mbingu na nchi; na yule nyumbu aliyekuwa chini yake akaenda mbele. 10 Basi mtu mmoja akaona hayo, akaenda akamwambia Yoabu, akasema, Tazama, mimi nalimwona Absalomu ametundikwa katika mwaloni. 11 Naye Yoabu akamwambia mtu yule aliyempasha habari, Je! Wewe umeona haya; Mbona, basi, hukumpiga hata nchi papo hapo? Nami ningalikupa fedha kumi na mshipi. 12 Yule mtu akamwambia Yoabu, Kama ningalipata fedha elfu mkononi mwangu, hata hivyo singalinyosha mkono wangu juu ya mwana wa mfalme; kwa maana mfalme masikioni mwetu alikuagiza wewe, na Abishai na Itai, akisema, Angalieni sana mtu awaye yote asimguse yule kijana, Absalomu. 13 Na tena, kama ningaliitendea roho yake kwa hila; (wala hapana neno lo lote liwezalo kufichwa mbele ya mfalme); ndipo wewe mwenyewe ungalijitenga. 14 Ndipo Yoabu akasema, Siwezi kungoja na kusema nawe hivi. Akachukua vyemba vitatu mkononi mwake, akamchoma Absalomu moyoni, alipokuwa akali hai katikati ya ule mwaloni. 15 Kisha vijana kumi, waliomchukulia Yoabu silaha zake wakamzunguka, wakampiga Absalomu, na kumwua. 16 Kisha Yoabu akapiga tarumbeta, wakarudi watu toka kuwafuatia Israeli; kwani Yoabu akawazuia watu. 17 Nao wakamtwaa Absalomu wakamtupa katika shimo kubwa mle msituni, wakaweka juu yake chungu kubwa sana la mawe; kisha Israeli wote wakakimbia kila mtu hemani mwake. 18 Huyo Absalomu alipokuwa yu hai alikuwa ameitwaa na kujiinulia ile nguzo iliyoko bondeni mwa mfalme; kwa maana alisema, Mimi sina mtoto wa kulikumbusha jina langu; akaiita hiyo nguzo kwa jina lake mwenyewe nayo inaitwa ziara la Absalomu hata hivi leo. 19 Basi Ahimaasi, mwana wa Sadoki, akasema, Niende mbio sasa, nikampelekee mfalme habari, jinsi Bwana alivyomlipiza kisasi juu ya adui zake. 20 Yoabu akamwambia, Wewe hutakuwa mchukua habari leo, siku nyingine utachukua habari; lakini leo hutachukua habari, kwa sababu mwana wa mfalme amekufa. 21 Ndipo Yoabu akamwambia Mkushi mmoja, Nenda ukamwambie mfalme hayo uliyoyaona. Na huyo Mkushi akajiinamisha mbele ya Yoabu, akaenda zake mbio. 22 Ndipo Ahimaasi, mwana wa Sadoki, akamwambia Yoabu mara ya pili, Haidhuru, tafadhali nipe ruhusa, nipige mbio na mimi nyuma ya huyo Mkushi. Naye Yoabu akasema, Mbona wewe unataka kupiga mbio, mwanangu, kwa maana hutapata kitu kwa habari hizo unazopeleka? 23 Akasema, Haidhuru, nitapiga mbio. Akamwambia, Haya, piga mbio. Ndipo Ahimaasi akapiga mbio, akishika njia ya uwandani, akampita yule Mkushi. 24 Basi Daudi alikuwa ameketi kati ya malango mawili; mlinzi akapanda juu hata dari ya lile lango hata ukutani, akainua macho yake, akaangalia, na tazama, mtu anakuja mbio peke yake. 25 Mlinzi akalia, akamwambia mfalme. Naye mfalme akasema, Kama yu peke yake, ana habari kinywani mwake. Akaja mbio, akakaribia. 26 Kisha huyo mlinzi akaona mtu mwingine anapiga mbio; mlinzi akamwita bawabu, akasema, Angalia, mtu mwingine anakuja mbio peke yake. Mfalme akasema, Huyu naye analeta habari. 27 Na huyo mlinzi akasema, Nionavyo mimi, kupiga mbio kwake yule wa kwanza ni kama kupiga mbio kwake Ahimaasi, mwana wa Sadoki. Naye mfalme akasema, Yeye ni mtu mwema, anakuja na habari njema. 28 Ahimaasi akainua sauti yake, akamwambia mfalme, Amani. Akainama mbele ya mfalme kifudifudi, akasema, Ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyewatoa watu hao walioiinua mikono yao juu ya bwana wangu, mfalme. 29 Mfalme akauliza, Je! Yule kijana, Absalomu, yu salama? Ahimaasi akajibu, Yoabu aliponituma mimi mtumishi wa mfalme, mimi mtumishi wako, naliona kishindo kikubwa, lakini sikujua sababu yake. 30 Naye mfalme akasema, Geuka, usimame hapa. Akageuka, akasimama. 31 Na tazama, yule Mkushi akafika; Mkushi akasema, Nina habari kwa bwana wangu mfalme; kwa maana Bwana amekulipizia kisasi leo juu ya hao wote walioinuka kupigana nawe. 32 Naye mfalme akamwambia yule Mkushi, Yule kijana, Absalomu, je! Yu salama? Yule Mkushi akajibu, Adui za bwana wangu mfalme, na wote wainukao ili kukudhuru, na wawe kama alivyo yule kijana. 33 Naye mfalme akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! Mwanangu Absalomu! Laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!

2 Samweli 19

1 Kisha Yoabu akaambiwa, Angalia, mfalme anamlilia Absalomu na kumwombolezea. 2 Na kushinda kwao vitani siku ile kukageuzwa kuwa maombolezo kwa watu wote; maana watu walisikia siku ile ya kwamba, Mfalme anahuzunika kwa ajili ya mwanawe. 3 Watu wakajificha siku ile, wakaingia mjini kama vile watu waonao fedheha wajifichavyo, hapo wakimbiapo vitani. 4 Mfalme akajifunika uso; na mfalme akalia kwa sauti kuu, Mwanangu Absalomu, Absalomu, mwanangu, mwanangu! 5 Basi Yoabu akaingia nyumbani kwa mfalme, akasema, Wewe leo umefedhehesha nyuso za watumishi wako wote, waliokuokoa leo roho yako, na roho za wanao, na za binti zako, na roho za wakezo, na roho za masuria wako; 6 kwa kuwa unawapenda wakuchukiao, na unawachukia wakupendao. Maana umetangaza leo ya kuwa wakuu na watumishi wako si kitu kwako; maana leo nimetambua hivi; kama Absalomu angaliishi, na sisi sote tungalikufa leo, ingalikuwa vyema machoni pako. 7 Basi sasa, ondoka, utoke nje, ukaseme na watumishi wako maneno ya kuwatuliza roho zao; maana mimi nakuapia kwa Bwana, usipotoka, hatabaki hata mtu mmoja pamoja nawe usiku huu; na mambo haya yatakuwa mabaya kwako kuliko mabaya yote yaliyokupata tokea ujana wako hata sasa. 8 Ndipo mfalme akaondoka, akaketi langoni. Nao wote wakaambiwa ya kwamba, Angalieni, mfalme ameketi langoni; watu wote wakaenda huko mbele ya mfalme. Basi, Israeli wote walikuwa wamekimbia kila mtu hemani kwake. 9 Wakashindana watu wote katika kabila zote za Israeli, wakisema, Mfalme alitutoa mikononi mwa adui zetu, akatuokoa mikononi mwa Wafilisti; naye sasa amekimbia kutoka nchi hii mbele ya Absalomu. 10 Na huyo Absalomu, tuliyemtia mafuta ili awe juu yetu, amekufa vitani. Basi sasa mbona ninyi hamsemi neno lo lote juu ya kumrudisha tena mfalme? 11 Naye mfalme Daudi akatuma kwa Sadoki na Abiathari, makuhani, kusema, Neneni na wazee wa Yuda, mkisema, Kwa nini ninyi mmekuwa wa mwisho wa kumrudisha tena mfalme nyumbani kwake? Kwa maana maneno ya Israeli wote yamemjia mfalme, ili kumleta nyumbani kwake. 12 Ninyi ni ndugu zangu, ninyi ni mfupa wangu na nyama yangu; mbona basi ninyi mmekuwa wa mwisho wa kumrudisha tena mfalme. 13 Kisha mkamwambie Amasa, Je! Si wewe uliye mfupa wangu, na nyama yangu? Mungu anifanyie hivyo, na kuzidi, usipokuwa wewe jemadari wa jeshi mbele yangu daima mahali pa Yoabu. 14 Akawainamisha mioyo watu wote wa Yuda, kama mtu mmoja; basi wakatuma kwa mfalme, Rudi wewe na watumishi wako wote. 15 Hivyo mfalme akarudi, akafika Yordani. Kisha Yuda wakaja Gilgali kwenda kumlaki mfalme, na kumvusha mfalme Yordani. 16 Akafanya haraka Shimei, mwana wa Gera, Mbenyamini, wa Bahurimu akashuka pamoja na watu wa Yuda ili kumlaki mfalme Daudi. 17 Na Watu elfu wa Benyamini walikuwa pamoja naye, na huyo Siba mtumwa, nyumba ya Sauli, na hao wanawe kumi na watano, na watumwa wake ishirini pamoja naye; wakavuka Yordani mbele ya mfalme. 18 Tena ikavuka mashua ili kuwavusha jamaa ya mfalme, na kufanya aliyoyaona kuwa mema. Ndipo Shimei, mwana wa Gera, akamwangukia mfalme alipokuwa amevuka Yordani. 19 Akamwambia mfalme, Bwana wangu asinihesabie uovu, wala usiyakumbuke yale niliyoyatenda mimi mtumwa wako kwa upotoe siku ile alipotoka Yerusalemu bwana wangu mfalme, hata mfalme ayatie moyoni mwake. 20 Kwa kuwa mimi mtumwa wako najua ya kwamba nimekosa; kwa hiyo, tazama, nimekuja leo, wa kwanza wa nyumba yote ya Yusufu, kushuka ili nimlaki bwana wangu mfalme. 21 Lakini Abishai, mwana wa Seruya, akajibu na kusema, Je! Shimei hatauawa kwa sababu hii, kwa kuwa amemlaani masihi wa BWANA? 22 Lakini Daudi akasema, Mimi nina nini nanyi, enyi wana wa Seruya, hata mmekuwa adui zangu leo? Je! Atauawa mtu ye yote leo katika Israeli? Kwa maana sijui mimi leo ya kwamba ndimi mfalme juu ya Israeli? 23 Kisha mfalme akamwambia Shimei, Hutakufa. Mfalme akamwapia. 24 Kisha Mefiboshethi, mwana wa Sauli, akashuka ili amlaki mfalme; alikuwa hakukata kucha za miguu yake wala kukata ndevu zake, wala kufua nguo zake, tangu siku alipoondoka mfalme, hata siku hiyo aliporudi kwake kwa amani. 25 Basi ikawa, alipofika Yerusalemu kumlaki mfalme, mfalme akamwambia, Mbona hukwenda pamoja nami, Mefiboshethi? 26 Naye akajibu, Bwana wangu, Ee mfalme, mtumwa wangu alinidanganya; kwa kuwa mimi mtumwa wako nilisema, Nitajitandikia punda, nipate kumpanda, na kwenda pamoja na mfalme; kwa sababu mimi mtumwa wako ni kiwete. 27 Naye amenisingizia mimi mtumwa wako kwa bwana wangu mfalme; lakini bwana wangu mfalme ni kama malaika wa Mungu; utende basi yaliyo mema machoni pako. 28 Kwa kuwa jamaa yote ya baba yangu walikuwa kama watu wa kufa tu mbele ya bwana wangu mfalme; ila uliniweka mimi mtumwa wako kati ya hao walao mezani pako. Basi ni haki gani sasa niliyo nayo, hata nimlilie mfalme zaidi? 29 Basi mfalme akamwambia, Kwa nini unazidi kuyanena mambo yako? Mimi naamua, Wewe na Siba mwigawanye hiyo nchi. 30 Naye Mefiboshethi akamwambia mfalme, Naam, hata yote na atwae yeye, kwa kuwa bwana wangu mfalme amekuja kwa amani nyumbani kwake. 31 Tena Barzilai, Mgileadi, akashuka kutoka Rogelimu; akavuka Yordani pamoja na mfalme, amvushe Yordani. 32 Naye huyo Barzilai alikuwa mzee sana, amepata umri wa miaka themanini; naye amemlisha mfalme hapo alipokuwapo Mahanaimu; kwa kuwa alikuwa mtu mwenye cheo kikubwa. 33 Naye mfalme akamwambia Barzilai, Uvuke pamoja nami; nami nitakulisha kwangu huko Yerusalemu. 34 Lakini Barzilai akamjibu mfalme, Siku ni ngapi za miaka ya maisha yangu, hata mimi nipande pamoja na mfalme kwenda Yerusalemu? 35 Nimepata leo miaka themanini; nami je! Naweza kupambanua mema na mabaya? Mimi mtumwa wako, je! Naweza kuonja nilacho au ninywacho? Naweza kusikia tena sauti ya waimbaji waume na wake? Kwa nini basi mtumwa wako amlemee bado bwana wangu mfalme? 36 Mtumwa wako ataka kuvuka Yordani tu pamoja na mfalme; tena mbona mfalme anilipie thawabu ya namna hii? 37 Niache nirudi basi, mimi mtumwa wako, ili nife katika mji wangu mwenyewe, karibu na kaburi la baba yangu na la mama yangu. Lakini tazama, mtumwa wako Kimhamu; na avuke yeye pamoja na bwana wangu mfalme; nawe ukamtendee yeye yaliyo mema machoni pako. 38 Mfalme akajibu, Haya, Kimhamu na avuke pamoja nami, nami nitamtendea yaliyo mema machoni pako wewe; na kila utakalotaka kwangu, mimi nitalifanya kwa ajili yako. 39 Basi watu wote wakavuka Yordani, naye mfalme akavuka; kisha mfalme akambusu Barzilai, akambariki; naye akarejea mahali pake. 40 Hivyo mfalme akavuka, akafika Gilgali; Kimhamu akavuka pamoja naye; na watu wote wa Yuda wakamvusha mfalme, na nusu ya watu wa Israeli. 41 Tena, angalia, watu wote wa Israeli wakamjia mfalme wakamwambia mfalme, Kwa nini ndugu zetu, watu wa Yuda wamekuiba, na kumvusha Yordani mfalme, na jamaa yake, na watu wote wa Daudi pamoja naye? 42 Ndipo watu wote wa Yuda wakawajibu hao watu wa Israeli, Ni kwa sababu mfalme ndiye wa jamaa yetu; mbona basi ninyi mmekasirika kwa ajili ya jambo hili? Je! Sisi tumekula kitu cha mfalme? Ama ametupa sisi zawadi yo yote? 43 Hao watu wa Israeli wakawajibu watu wa Yuda, wakasema, Sisi tunazo sehemu kumi katika mfalme, tena tunayo haki yetu katika Daudi zaidi kuliko ninyi; mbona basi ninyi mmetudharau sisi, lisitakwe kwanza shauri letu katika kumrudisha tena mfalme wetu? Na maneno ya watu wa Yuda yakawa makali kuliko maneno ya watu wa Israeli.

2 Samweli 20

1 Basi ilitukia ya kwamba kulikuwapo mtu asiyefaa, jina lake akiitwa Sheba, mwana wa Bikri, Mbenyamini; naye akapiga tarumbeta, akasema, Sisi hatuna sehemu katika Daudi, wala hatuna urithi katika mwana wa Yese; nendeni kila mtu hemani kwake, enyi Israeli. 2 Basi wakapanda watu wote wa Israeli kutoka kumfuata Daudi, wakamfuata Sheba, mwana wa Bikri; lakini watu wa Yuda wakaambatana na mfalme wao, toka Yordani hata kufika Yerusalemu. 3 Basi Daudi akaja Yerusalemu nyumbani kwake; kisha mfalme akawatwaa wale wanawake kumi, masuria, aliowaacha kuitunza nyumba, akawatia nyumbani mwa kulindwa, akawalisha, ila asiingie kwao. Basi wakafungwa hata siku ya kufa kwao, huku wakiishi hali ya ujane. 4 Ndipo mfalme akamwambia Amasa, Uwakusanye pamoja kwangu kwa siku tatu watu wa Yuda, na uwepo wewe hapa. 5 Amasa akaenda kuwakusanya Yuda; lakini akakawia zaidi ya huo muda aliowekewa. 6 Basi Daudi akamwambia Abishai, Sasa Sheba, mwana wa Bikri, atatudhuru, kuliko Absalomu; twaa wewe watumishi wa bwana wako, ukamfuatie, asiingie katika miji yenye boma, na kujiponya machoni petu. 7 Ndipo wakatoka nyuma yake watu wa Yoabu, na Wakerethi na Wapelethi, na mashujaa wote; wakatoka Yerusalemu, ili kumfuatia Sheba, mwana wa Bikri. 8 Basi walipokuwako kwenye lile jiwe kubwa lililoko Gibeoni, Amasa akaja kuwalaki. Naye Yoabu alikuwa amefungwa mavazi yake ya vita aliyoyavaa, na juu yake alikuwa na mshipi, na upanga uliotiwa viunoni mwake ndani ya ala yake; naye alipokuwa akiendelea, ukaanguka. 9 Naye Yoabu akamwambia Amasa, Amani kwako, ndugu yangu. Kisha Yoabu akamshika Amasa ndevu kwa mkono wake wa kuume ili ambusu. 10 Wala Amasa hakuangalia huo upanga uliomo mkononi mwa Yoabu; basi akampiga nao wa tumbo, akamwaga matumbo yake chini, asimpige mara ya pili; naye akafa. Kisha Yoabu na Abishai, nduguye, wakamfuata Sheba, mwana wa Bikri. 11 Akasimama karibu naye mmojawapo wa vijana wa Yoabu, huyo akasema, Ampendaye Yoabu, na aliye wa Daudi, na amfuate Yoabu. 12 Lakini Amasa alikuwa anagaagaa katika damu yake katikati ya njia kuu. Basi yule mtu alipowaona watu wote wamesimama, akamwondoa Amasa toka njia kuu akamtia kondeni, akamfunika nguo, hapo alipoona ya kuwa kila mtu aliyefika kwake amesimama. 13 Na alipoondolewa katika njia kuu, watu wote wakapita, wakamwandama Yoabu ili kumfuatia Sheba, mwana wa Bikri. 14 Naye akapita kati ya kabila zote za Israeli mpaka Abeli, na kwa Bethmaaka na Wabikri wote; nao wakakusanyika, wakaenda pia kumwandama. 15 Na hao wakaja wakamhusuru katika Abeli wa Bethmaaka, wakafanya chuguu mbele ya mji, nayo ikasimama kuielekea ngome; na watu wote waliokuwa pamoja na Yoabu wakavunja-vunja ukuta, wapate kuubomoa. 16 Ndipo akalia mwanamke mmoja mwenye akili toka mjini, Sikieni, sikieni; mwambieni na Yoabu, aje hapa karibu, niseme naye. 17 Basi akamkaribia; na yule mwanamke akasema, Ndiwe Yoabu? Akajibu, Ndimi. Ndipo akamwambia Sikia maneno ya mjakazi wako. Akajibu, Mimi nasikia. 18 Kisha akanena, akisema, Watu hunena zamani za kale, wakisema, Wasikose kuuliza huko Abeli; ndivyo walivyomaliza shauri. 19 Mimi ni wa hao wenye amani, walio waaminifu katika Israeli; wewe unatafuta kuuharibu mji, na mama wa Israeli; mbona wataka kuumeza urithi wa Bwana? 20 Yoabu akajibu, akasema, Isiwe, isiwe kwangu, niumeze wala kuuharibu. 21 Neno hili silo hivyo; lakini mtu mmoja wa milima ya Efraimu, Sheba, mwana wa Bikri, jina lake, ameinua mkono wake juu ya mfalme, naam, Daudi, basi mtoeni yeye tu, nami nitaondoka katika mji huu. Basi yule mwanamke akamwambia Yoabu, Tazama, kichwa chake utatupiwa juu ya ukuta. 22 Ndipo yule mwanamke akawaendea watu wote katika akili zake. Nao wakamkata kichwa Sheba, mwana wa Bikri, wakamtupia Yoabu huko nje. Ndipo akapiga tarumbeta, nao wakatawanyika kutoka mjini kila mtu hemani kwake. Naye Yoabu akarudi mpaka Yerusalemu kwa mfalme. 23 Basi Yoabu alikuwa juu ya jeshi lote la Israeli; na Benaya, mwana wa Yehoyada, alikuwa juu ya Wakerethi, na juu ya Wapelethi; 24 na Adoramu alikuwa juu ya shokoa; na Yehoshafati, mwana wa Ahiludi, alikuwa mkumbushi; 25 na Shausha mwandishi; na Sadoki na Abiathari walikuwa makuhani. 26 Tena na Ira, Myairi, alikuwa kuhani kwa Daudi.

2 Samweli 21

1 Kulikuwa na njaa siku za Daudi muda wa miaka mitatu, mwaka kwa mwaka; naye Daudi akautafuta uso wa Bwana. Bwana akasema, Ni kwa ajili ya Sauli, na kwa nyumba yake yenye damu, kwa kuwa aliwaua hao Wagibeoni. 2 Ndipo mfalme akawaita Wagibeoni akawaambia; (basi Wagibeoni si wa wana wa Israeli, ila ni wa masalio ya Waamori; na wana wa Israeli walikuwa wamewaapia; lakini Sauli akatafuta kuwaua katika juhudi yake kwa ajili ya wana wa Israeli na Yuda;) 3 basi Daudi akawaambia hao Wagibeoni, Niwatendee nini? Na kwa tendo gani nifanye upatanisho, mpate kuubariki urithi wa Bwana? 4 Na hao Wagibeoni wakamwambia, Si jambo la fedha wala dhahabu lililo kati ya sisi na Sauli, au nyumba yake; wala si juu yetu kumwua mtu ye yote katika Israeli. Akasema Mtakayoyanena, ndiyo nitakayowatendea ninyi. 5 Wakamwambia mfalme, Yule mtu aliyetupoteza, na kutufanyia shauri la kutuharibu, tusikae katika mipaka yo yote ya Israeli, 6 basi, na tutolewe watu saba katika wanawe, nasi tutawatundika mbele za Bwana katika Gibeoni, katika mlima wa Bwana. Mfalme akasema, Nitawatoa. 7 Lakini mfalme akamwachilia Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli, kwa ajili ya kiapo cha Bwana kilichokuwa kati yao, yaani, kati ya Daudi na Yonathani, mwana wa Sauli. 8 Ila mfalme akawatwaa hao wana wawili wa Rispa, binti Aya, aliomzalia Sauli, Armoni na Mefiboshethi; na wana watano wa Merabu binti Sauli, aliomzalia Adrieli, mwana wa Barzilai, Mmeholathi; 9 akawatia mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele za Bwana, nao wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za mavuno, za kwanza, mwanzo wa mavuno ya shayiri. 10 Naye Rispa, binti Aya, akatwaa nguo ya magunia akajitandikia mwambani, tangu mwanzo wa mavuno hata waliponyeshewa mvua toka mbinguni; wala hakuacha ndege wa angani kukaa juu yao mchana, wala wanyama wa mwitu usiku. 11 Kisha akaambiwa Daudi hayo aliyoyafanya huyo Rispa binti Aya, suria wa Sauli. 12 Akaenda Daudi, akaitwaa mifupa ya Sauli na mifupa ya Yonathani mwanawe mikononi mwa watu wa Yabesh-gileadi; waliyoiiba katika njia ya Bethshani, hapo Wafilisti walipowatungika, katika siku hiyo waliyomwua Sauli huko Gilboa; 13 naye akaileta toka huko hiyo mifupa ya Sauli, na mifupa ya Yonathani mwanawe; nao wakaizoa mifupa yao waliotundikwa. 14 Kisha wakaizika mifupa ya Sauli na ya Yonathani mwanawe katika nchi ya Benyamini, huko Zela, kaburini mwa Kishi babaye; wakafanya yote aliyoyaamuru mfalme. Na baadaye Mungu aliiridhia hiyo nchi. 15 Basi kulikuwa na vita tena kati ya Wafilisti na Israeli; Daudi akashuka mpaka Gobu, na watumishi wake pamoja naye, akapigana na Wafilisti; naye Daudi akaishiwa na nguvu. 16 Naye Ishi-benobu, aliyekuwa mmojawapo wa Warefai, ambaye uzito wa mkuki wake ulikuwa shekeli mia tatu za shaba kwa uzani ,naye amejifungia upanga mpya,alijaribu kumwua Daudi. 17 Lakini Abishai, mwana wa Seruya, akamsaidia, akampiga Mfilisti, akamwua. Ndipo watu wa Daudi wakamwapia, wakasema, Wewe hutatoka tena pamoja nasi kwenda vitani, usije ukaizima taa ya Israeli. 18 Ikawa baada ya hayo, kulikuwa na vita tena na Wafilisti huko Gobu; ndipo Sibekai, Mhushathi, alipomwua Safu, aliyekuwa mmojawapo wa Warefai. 19 Kulikuwa na vita tena na Wafilisti huko Gobu; na Elhanani, mwana wa Yairi, Mbethlehemi, alimwua Goliathi, Mgiti, ambaye mti wa mkuki wake ulikuwa kama mti wa mfumaji. 20 Kulikuwa na vita tena huko Gathi; ambako kulikuwa na mtu mrefu sana, mwenye vidole sita katika kila mkono, na vidole sita katika kila mguu, jumla yake ishirini na vinne; yeye naye alizaliwa kwa Mrefai. 21 Naye huyo alipowatukana Israeli, ndipo Yonathani, mwana wa Shama, nduguye Daudi, akamwua. 22 Hao wanne walizaliwa kwake huyo Mrefai wa Gathi; wakaanguka kwa mkono wa Daudi, na kwa mikono ya watumishi wake.

2 Samweli 22

1 Basi Daudi akamwambia Bwana maneno ya wimbo huu, siku ile Bwana alipomwokoa mikononi mwa adui zake zote, na mkononi mwa Sauli; 2 akasema, Bwana ndiye jabali langu, na ngome yangu, na mwokozi wangu, naam, wangu; 3 Mungu wa mwamba wangu, nitamwamini yeye; Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, mnara wangu, na makimbilio yangu; Mwokozi wangu, waniokoa na jeuri. 4 Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa; Hivyo nitaokoka na adui zangu. 5 Maana mawimbi ya mauti yalinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu. 6 Kamba za kuzimu zilinizunguka; Mitego ya mauti ikanikabili. 7 Katika shida yangu nalimwita Bwana, Naam, nikamlalamikia Mungu wangu; 8 Ndipo nchi ilipotikisika na kutetemeka, Misingi ya mbinguni ikasuka-suka Na kutikisika, kwa sababu alikuwa na ghadhabu. 9 Kukapanda moshi kutoka puani mwake, Moto ukatoka kinywani mwake ukala; Makaa yakawashwa nao. 10 Aliziinamisha mbingu akashuka; Kukawa na giza kuu chini ya miguu yake. 11 Akapanda juu ya kerubi akaruka; Naam, alionekana juu ya mabawa ya upepo. 12 Akafanya giza hema zake za kumzunguka, Makusanyiko ya maji, mawingu makuu ya mbinguni. 13 Toka mwangaza uliokuwa mbele zake Makaa ya moto yakawashwa. 14 Bwana alipiga radi toka mbinguni, Naye Aliye juu akaitoa sauti yake. 15 Akapiga mishale, akawatawanya; Umeme, naye akawatapanya. 16 Ndipo ilipoonekana mikondo ya bahari, Misingi ya ulimwengu ikafichuliwa, Kwa kukemea kwake Bwana, Kwa mvumo wa pumzi ya puani mwake. 17 Alipeleka kutoka juu, akanishika; Akanitoa katika maji mengi; 18 Akaniokoa na adui yangu mwenye nguvu, Na wale walionichukia; Maana walikuwa na nguvu kuliko mimi. 19 Walinikabili siku ya msiba wangu; Lakini Bwana alikuwa tegemeo langu. 20 Akanitoa akanipeleka panapo nafasi; Aliniponya kwa kuwa alipendezwa nami. 21 Bwana alinitendea sawasawa na haki yangu; Sawasawa na usafi wa mikono yangu akanilipa. 22 Maana nimezishika njia za Bwana, Wala sikumwasi Mungu wangu. 23 Maana hukumu zake zote zilikuwa mbele yangu; Na kwa habari za amri zake, sikuziacha. 24 Nami nalikuwa mkamilifu kwake, Nikajilinda na uovu wangu. 25 Basi Bwana amenilipa sawasawa na haki yangu; Sawasawa na usafi wa mikono yangu mbele zake. 26 Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili Kwa mkamilifu utajionyesha kuwa mkamilifu; 27 Kwake ajitakasaye utajionyesha kuwa mtakatifu; Na kwa mpotovu utajionyesha kuwa mkaidi. 28 Na watu wanaoonewa wewe utawaokoa; Ila macho yako ni juu ya wenye kiburi, uwadhili. 29 Kwa kuwa wewe u taa yangu, Ee Bwana; Na Bwana ataniangazia giza langu. 30 Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi; Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta. 31 Mungu njia yake ni kamilifu; Ahadi ya Bwana imehakikishwa; Yeye ndiye ngao yao Wote wanaomkimbilia. 32 Maana ni nani aliye Mungu, ila Bwana? Ni nani aliye mwamba, ila Mungu wetu? 33 Mungu ndiye ngome yangu yenye nguvu; Naye huwaongoza wakamilifu katika njia yake. 34 Huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu; Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. 35 Ananifundisha mikono yangu vita; Hata mikono yangu yaupinda upinde wa shaba. 36 Nawe umenipa ngao ya wokovu wako; Na unyenyekevu wako umenikuza. 37 Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Wala miguu yangu haikuteleza. 38 Nimewafuatia adui zangu, na kuwaangamiza; Wala sikurudi nyuma hata walipokomeshwa. 39 Nami nimewakomesha na kuwapiga-piga wasiweze kusimama; Naam, wameanguka chini ya miguu yangu. 40 Maana umenifunga mshipi wa nguvu kwa vita; Umenitiishia chini yangu walioniondokea. 41 Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Ili niwakatilie mbali wanaonichukia. 42 Walitazama, lakini hakuna wa kuokoa; Walimwita Bwana, lakini hakuwajibu. 43 Ndipo nikawaponda kama mavumbi ya nchi, Nikawakanyaga kama matope ya njiani, nikawatawanya. 44 Nawe umeniokoa na mashindano ya watu wangu; Umenihifadhi niwe kichwa cha mataifa; Watu nisiowajua watanitumikia. 45 Wageni watanijia wakinyenyekea; Kwa kusikia tu habari zangu, Mara watanitii. 46 Wageni nao watatepetea, Watatoka katika ngome zao wakitetemeka. 47 Bwana ndiye aliye hai; Na ahimidiwe mwamba wangu; Na atukuzwe Mungu wa mwamba wa wokovu wangu; 48 Naam, Mungu anipatiaye kisasi, Na kuwatweza watu chini yangu, 49 Na kunileta nje nitoke kwa adui zangu; Naam, waniinua juu yao walioniinukia; Waniponya na mtu wa jeuri. 50 Basi, Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa, Nami nitaliimbia jina lako. 51 Ampa mfalme wake wokovu mkuu; Amfanyia fadhili masihi wake Daudi na mzao wake ,hata milele.

2 Samweli 23

1 Basi haya ndiyo maneno ya mwisho ya Daudi. Daudi, mwana wa Yese, anena, Anena huyo mtu aliyeinuliwa juu, Yeye, masihi wake Mungu wa Yakobo,Mtungaji wa nyimbo za Israeli mwenye kupendeza; 2 Roho ya Bwana ilinena ndani yangu, Na neno lake likawa ulimini mwangu. 3 Mungu wa Israeli alisema, Mwamba wa Israeli aliniambia, Atawalaye wanadamu kwa haki, Akitawala katika kicho cha Mungu, 4 Atakuwa kama nuru ya asubuhi jua lichapo, Asubuhi isiyo na mawingu. 5 Je! Sivyo ilivyo nyumba yangu mbele za Bwana? Kwa kuwa amefanya nami agano la milele; Ina taratibu katika yote, ni thabiti, Maana ni wokovu wangu wote, na shauku langu lote. 6 Lakini hatawachipuza watu wa ubatili; Watakuwa wote kama miiba ya nyikani ya kutupwa, Ambayo haivuniki kwa mkono, 7 Mtu atakayeigusa hiyo, Na awe na chuma na mpini wa mkuki, Nao watateketezwa papo hapo kwa moto. 8 Haya ndiyo majina ya mashujaa aliokuwa nao Daudi; Yashobeamu Mhakmoni,mkuu wa maakida ;huyo aliliinua shoka lake juu ya watu mia nane waliouawa pamoja. 9 Na baada yake kulikuwa na Eleazari, mwana wa Dodai, Mwahohi, mmojawapo wa wale mashujaa watatu waliokuwa pamoja na Daudi; walipowatukana Wafilisti waliokuwa wamekusanyika huko ili kupigana, na watu wa Israeli walikuwa wamekwenda zao; 10 huyo aliinuka, akawapiga Wafilisti hata mkono wake ukachoka, na mkono wake ukaambatana na upanga; naye Bwana akafanya wokovu mkuu siku ile; nao watu wakarudi nyuma yake ili kuteka nyara tu. 11 Na baada yake kulikuwa na Shama, mwana wa Agee, Mharari; nao Wafilisti walikuwa wamekusanyika huko Lehi, palipokuwapo konde lililojaa midengu; nao watu wakawakimbia Wafilisti; 12 ila huyo alisimama katikati ya konde lile, akalipigania, akawaua Wafilisti; naye Bwana akafanya wokovu mkuu. 13 Tena, watatu miongoni mwa wale thelathini waliokuwa wakuu wakashuka, wakamwendea Daudi wakati wa mavuno mpaka pango la Adulamu, na kikosi cha Wafilisti walikuwa wamefanya kambi katika bonde la Warefai. 14 Naye Daudi wakati ule alikuwako ngomeni, na jeshi la Wafilisti wakati ule walikuwako Bethlehemu. 15 Daudi akatamani, akasema, Laiti mtu angeninywesha maji ya kisima cha Bethlehemu, kilicho karibu na lango! 16 Basi hao mashujaa watatu wakapenya jeshi la Wafilisti, wakateka maji kutoka kile kisima cha Bethlehemu, kilicho karibu na lango, wakayachukua, wakamletea Daudi; walakini yeye hakukubali kuyanywa, akayamimina mbele za Bwana. 17 Akasema, Hasha, Bwana, nisifanye hivi; je! Si damu hii ya watu hao waliohatirisha nafsi zao? Kwa hiyo hakukubali kuyanywa. Hayo ndiyo waliyoyafanya wale mashujaa watatu. 18 Tena, Abishai, nduguye Yoabu, mwana wa Seruya, alikuwa mkuu wa wale watatu. Huyo aliuinua mkuki wake juu ya watu mia tatu, akawaua, akawa na jina kati ya wale watatu. 19 Je! Huyo hakuwa na heshima maalumu miongoni mwa wale watatu? Kwa hiyo akawekwa kuwa akida wao; ila hakudiriki kuwamo katika wale watatu. 20 Tena Benaya, mwana wa Yehoyada, mtu hodari wa Kabseeli aliyekuwa amefanya mambo makuu; aliwaua simba wakali wawili wa Moabu, pia akashuka akamwua simba katikati ya shimo wakati wa theruji. 21 huyo naye akamwua Mmisri, mtu mrefu; naye huyo Mmisri alikuwa na mkuki mkononi; lakini yeye alimshukia na gongo, akamnyakulia Mmisri mkuki mkononi mwake, akamwua kwa mkuki wake mwenyewe. 22 Hayo ndiyo aliyoyafanya Benaya, mwana wa Yehoyada, akawa na jina kati ya wale mashujaa watatu. 23 Alikuwa mwenye heshima kuliko wale thelathini, ila hakudiriki kuwamo katika wale watatu. Naye Daudi akamweka juu ya walinzi wake. 24 Asaheli, nduguye Yoabu, alikuwa mmojawapo wa wale thelathini; na Elhanani, mwana wa Dodo, wa Bethlehemu; 25 na Shama, Mharodi, na Elika, Mharodi; 26 na Helesi, Mpeloni, na Ira, mwana wa Ikeshi, Mtekoi; 27 na Abiezeri, Mwanathothi, na Sibekai, Mhushathi; 28 na Salmoni, Mwahohi, na Maharai, Mnetofathi; 29 na Heledi, mwana wa Baana, Mnetofathi, na Itai, mwana wa Ribai, wa Gibea wa wana wa Benyamini; 30 na Benaya, Mpirathoni, na Hurai, wa vijito vya Gaashi; 31 na Abieli, Mwarbathi, na Azmawethi, Mbarhumi; 32 na Eliaba, Mshaalboni, na wana wa Yasheni; na Yonathani, 33 mwana wa Shama, Mharari, na Ahiamu, mwana wa Shalali, Mharari; 34 na Elifeleti, mwana wa Ahasbai, na Heferi, Mmaakathi, na Eliamu, mwana wa Ahithofeli, Mgiloni; 35 na Hezro, Mkarmeli, na Paarai, Mwarbi; 36 na Igali, mwana wa Nathani, wa Soba, na Bani, Mgadi; 37 na Seleki, Mwamoni, na Naharai, Mbeerothi, ambao ni wachukua silaha wa Yoabu, mwana wa Seruya; 38 na Ira, Mwithri, na Garebu, Mwithri; 39 na Uria, Mhiti; jumla yao ilikuwa watu thelathini na saba.

2 Samweli 24

1 Tena hasira ya Bwana ikawaka juu ya Israeli, akamtia Daudi nia juu yao, akisema, Nenda, ukawahesabu Israeli na Yuda. 2 Basi mfalme akamwambia Yoabu, jemadari wa jeshi la askari, waliokuwa pamoja naye, Zunguka sasa katikati ya kabila zote za Israeli, tangu Dani mpaka Beer-sheba, mkawahesabu watu, nipate kujua jumla ya hao watu. 3 Naye Yoabu akamwambia mfalme, Bwana, Mungu wako, na awaongeze watu, hesabu yao ikiwa yo yote, mara mia, tena macho ya bwana wangu mfalme na yawaone; ila kwa nini neno hili limempendeza bwana wangu mfalme? 4 Lakini neno la mfalme likawa na nguvu juu ya Yoabu, na juu ya majemadari wa jeshi. Basi Yoabu akatoka na majemadari wa jeshi machoni pa mfalme, kwenda kuwahesabu watu wa Israeli. 5 Wakavuka Yordani, wakapiga kambi huko Aroeri, upande wa kuume wa mji ulioko kati ya bonde la Gadi, na mpaka Yazeri; 6 kisha wakaja Gileadi, na nchi ya Wahiti huko Kadeshi; kisha wakaja Dani, na kutoka Dani wakazunguka mpaka Sidoni, 7 wakaja ngomeni kwa Tiro, na kwa miji yote ya Wahivi, na ya Wakanaani; tena wakatoka kusini kwa Yuda huko Beer-sheba. 8 Nao walipokwisha kuzunguka nchi yote, wakaja Yerusalemu mwisho wa miezi kenda na siku ishirini. 9 Naye Yoabu akamtolea mfalme jumla ya hesabu ya watu; nao walikuwa wa Israeli mashujaa wenye kufuta panga mia nane elfu; nao wa Yuda walikuwa watu mia tano elfu. 10 Ndipo moyo wake Daudi ukamchoma baada ya kuwahesabu hao watu. Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya; lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa. 11 Na Daudi alipoondoka asubuhi, neno la Bwana likamjia nabii Gadi, mwonaji wake Daudi, kusema, 12 Nenda, ukanene na Daudi, Bwana asema hivi, Nakuwekea mambo matatu; katika haya uchague moja, nikutendee hilo. 13 Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza, akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma. 14 Naye Daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu. 15 Basi Bwana akawaletea Israeli tauni tangu asubuhi hata wakati ulioamriwa; nao wakafa watu toka Dani mpaka Beer-sheba sabini elfu. 16 Lakini huyo malaika aliponyosha mkono wake kuelekea Yerusalemu ili auharibu, Bwana akaghairi katika mabaya, akamwambia huyo malaika mwenye kuwaharibu watu, Yatosha, sasa ulegeze mkono wako. Naye yule malaika wa Bwana alikuwako karibu na kiwanja cha kupuria cha Arauna, Myebusi. 17 Daudi, alipomwoma malaika aliyewapiga watu, akanena na Bwana, akasema, Tazama, ni mimi niliyekosa, ni mimi niliyepotoka; lakini kondoo hawa, wamefanya nini? Mkono wako na uwe juu yangu, na juu ya nyumba ya baba yangu. 18 Siku hiyo Gadi akamwendea Daudi, akamwambia, Haya! Kwea wewe, ukamwinulie Bwana madhabahu penye kiwanja cha Arauna, Myebusi. 19 Basi Daudi akakwea sawasawa na neno la Gadi, kama Bwana alivyoamuru. 20 Huyo Arauna akatazama, akamwona mfalme na watumishi wake wakimjia; Arauna akatoka, akasujudu mbele ya mfalme kifulifuli hata nchi. 21 Arauna akasema, Bwana wangu mfalme amemjia mtumwa wake kwa kusudi gani? Naye Daudi akasema, Makusudi ninunue kwako kiwanja hiki, ili nimjengee Bwana madhabahu, ili kwamba tauni ipate kuzuiliwa katika watu. 22 Arauna akamwambia Daudi, Bwana wangu mfalme na akitwae, akatolee yaliyo mema machoni pake; tazama, ng'ombe hawa kwa sadaka ya kuteketezwa, tena vyombo vya kupuria, na vyombo vya ng'ombe, viko kwa kuni, 23 vitu hivi vyote, Ee mfalme, mimi Arauna nakupa wewe mfalme. Kisha Arauna akamwambia mfalme, Bwana, Mungu wako, na akukubali. 24 Lakini mfalme akamwambia Arauna, La, sivyo; lakini kweli nitavinunua kwako kwa thamani yake; wala sitamtolea Bwana, Mungu wangu, sadaka za kuteketezwa nisizozigharimia. Hivyo Daudi akakinunua hicho kiwanja cha kupuria na wale ng'ombe kwa shekeli hamsini za fedha. 25 Naye Daudi akamjengea Bwana madhabahu huko, akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Basi Bwana aliiridhia nchi, na tauni ikazuiliwa katika Israeli.

1 Wafalme 1

1 Mfalme Daudi alikuwa mzee, mkongwe katika siku zake, nao wakamfunika nguo, lakini asipate moto. 2 Kwa hiyo watumishi wake wakamwambia, Bwana wangu mfalme na atafutiwe kijana mwanamwali; naye asimame mbele ya mfalme, amtunze; alale kifuani mwako, ili bwana wangu mfalme apate moto. 3 Basi wakatafuta kijana mzuri mipakani mwote mwa Israeli, wakamwona Abishagi, Mshunami, wakamleta kwa mfalme. 4 Naye kijana huyo alikuwa mzuri sana; akamtunza mfalme, akamtumikia; walakini mfalme hakumjua. 5 Ndipo Adonia mwana wa Hagithi akatakabari, akasema, Mimi nitakuwa mfalme. Akajiwekea tayari magari na wapanda farasi, na watu hamsini wapige mbio mbele yake. 6 Tena baba yake hakumchukiza wakati wo wote kwa kusema, Mbona umefanya hivi? Kisha, alikuwa mtu mzuri sana; naye alizaliwa baada ya Absalomu. 7 Akashauriana na Yoabu, mwana wa Seruya, na Abiathari, kuhani; nao wakamsaidia Adonia, wakamfuata. 8 Ila Sadoki, kuhani, na Benaya, mwana wa Yehoyada, na Nathani, nabii, na Shimei, na Rei, na mashujaa wa Daudi, hao hawakuwa pamoja na Adonia. 9 Adonia akachinja kondoo, na ng'ombe, na vinono, karibu na jiwe la Zohelethi, lililo karibu na chemchemi Rogeli; akawaita ndugu zake wote, wana wa mfalme, na watu wote wa Yuda, watumishi wa mfalme; 10 ila Nathani, nabii, na Benaya, na mashujaa, na Sulemani nduguye, hakuwaita hao. 11 Ndipo Nathani akamwambia Bath-sheba, mamaye Sulemani, akasema, Je! Hukusikia ya kuwa Adonia, mwana wa Hagithi, anamiliki, na bwana wetu Daudi hana habari? 12 Haya basi, nikupe shauri, tafadhali, upate kuiokoa roho yako, na roho ya mwanao Sulemani. 13 Enenda uingie ndani kwa mfalme Daudi, ukamwambie, Je! Hukuniapia mimi mjakazi wako, Ee mfalme, bwana wangu, kusema, Hakika yake Sulemani mwana wako atamiliki baada yangu, na kuketi katika kiti changu cha enzi? Mbona basi anamiliki Adonia? 14 Tazama, wakati ule utakapokuwa katika kusema na mfalme, mimi nami nitaingia nyuma yako, na kuyahakikisha maneno yako. 15 Basi Bath-sheba akaingia ndani kwa mfalme, ndani ya chumba chake; naye mfalme alikuwa mzee sana; na Abishagi, Mshunami, alikuwa akimtumikia mfalme. 16 Bath-sheba akainama, akamsujudia mfalme. Naye mfalme akamwuliza, Wataka nini? 17 Akamwambia, Bwana wangu, uliniapia mimi mjakazi wako kwa Bwana, Mungu wako, ya kwamba, bila shaka Sulemani mwanao atamiliki baada yangu, yeye ndiye atakayeketi katika kiti changu cha enzi. 18 Na sasa, angalia, Adonia anamiliki; na wewe, bwana wangu mfalme, huna habari. 19 Tena amechinja ng'ombe, na vinono, na kondoo tele, na kuwaita wana wa mfalme wote pia, na Abiathari, kuhani, na Yoabu, jemadari wa jeshi. Ila Sulemani, mtumishi wako, huyu hakumwita. 20 Ee mfalme, bwana wangu, macho ya Israeli wote yanakuelekea wewe, kwamba uwaambie ni nani atakayeketi katika kiti chako cha enzi baada yako, Ee mfalme, bwana wangu. 21 Ama sivyo itakuwa, bwana wangu mfalme atakapolala pamoja na baba zake, mimi na mwanangu Sulemani tutahesabiwa kuwa wahalifu. 22 Basi tazama, alipokuwa katika kusema na mfalme, Nathani, nabii, aliingia. 23 Wakamwambia mfalme wakasema, Tazama, Nathani, nabii. Naye alipoingia ndani mbele ya mfalme, akamsujudia kifudifudi. 24 Nathani akasema, Ee mfalme, bwana wangu, je! Wewe umesema ya kwamba, Adonia atamiliki baada yangu, ndiye atakayeketi katika kiti changu cha enzi? 25 Maana leo ameshuka, na kuchinja ng'ombe, na vinono, na kondoo tele, naye amewaita wana wote wa mfalme, na majemadari wa jeshi, na Abiathari, kuhani; na tazama, wanakula na kunywa mbele yake, wakisema, Na aishi mfalme Adonia! 26 Walakini mimi, mimi mtumishi wako, na Sadoki, kuhani, na Benaya, mwana wa Yehoyada, na Sulemani, mtumishi wako, hakutuita sisi. 27 Je! Bwana wangu mfalme ndiye aliyelitenda jambo hili, bila kutujulisha sisi watumishi wako ni nani atakayeketi katika kiti cha enzi cha bwana wangu mfalme baada yake? 28 Ndipo mfalme Daudi akajibu, akasema, Niitieni Bath-sheba. Basi akaingia ndani kwa mfalme, akasimama mbele ya mfalme. 29 Naye mfalme akaapa, akasema, Bwana aishivyo, aliyenikomboa roho yangu katika shida zote, 30 hakika yake nitafanya leo kama vile nilivyokuapia kwa Bwana, Mungu wa Israeli, nikasema, Kwa yakini Sulemani mwanao atamiliki baada yangu, naye ndiye atakayeketi katika kiti changu cha enzi badala yangu. 31 Ndipo Bath-sheba akainama kifudifudi, akamsujudia mfalme, akasema, Bwana wangu mfalme Daudi na aishi milele. 32 Naye mfalme Daudi akasema, Niitie Sadoki, kuhani, na Nathani, nabii, na Benaya, mwana wa Yehoyada. Nao wakaingia ndani mbele ya mfalme. 33 Naye mfalme akawaambia, Twaeni pamoja nanyi watumishi wa bwana wenu, mkampandishe Sulemani mwanangu juu ya nyumbu wangu mimi mkamtelemshe mpaka Gihoni; 34 kisha Sadoki, kuhani, na Nathani, nabii, na wamtie mafuta huko, awe mfalme juu ya Israeli; kapigeni panda, mkaseme, Mfalme Sulemani na aishi! 35 Kisha pandeni juu nyuma yake, naye atakuja ili aketi katika kiti changu cha enzi; kwa maana atakuwa mfalme badala yangu; ndiye niliyemweka awamiliki Israeli na Yuda. 36 Basi Benaya, mwana wa Yehoyada, akamjibu mfalme, akasema, Amina; Bwana, Mungu na bwana wangu mfalme, na aseme vivyo hivyo. 37 Kama vile Bwana alivyokuwa pamoja na bwana wangu mfalme, kadhalika na awe pamoja na Sulemani, na kufanya kiti chake cha enzi kuwa kitukufu kuliko kiti cha enzi cha bwana wangu mfalme Daudi. 38 Basi wakashuka Sadoki, kuhani, na Nathani, nabii, na Benaya, mwana wa Yehoyada, na Wakerethi, na Wapelethi, wakampandisha Sulemani juu ya nyumbu wa mfalme Daudi, wakampeleka mpaka Gihoni. 39 Na Sadoki, kuhani, akatwaa ile pembe ya mafuta katika Hema, akamtia Sulemani mafuta. Nao wakapiga panda; na watu wote wakasema, Mfalme Sulemani na aishi! 40 Kisha watu wote wakapanda juu nyuma yake, watu wakapiga mazomari, wakafurahi furaha kubwa mno, hata nchi ikapasuka kwa sauti zao. 41 Basi Adonia, na wageni wote waliokuwa pamoja naye, wakasikia hayo walipokuwa wamekwisha kula. Naye Yoabu aliposikia sauti ya panda alisema, Za nini kelele hizi za mji uliotaharuki? 42 Naye alipokuwa katika kunena, tazama Yonathani, mwana wa Abiathari kuhani, akafika. Naye Adonia akasema, Karibu; maana wewe u mtu mwema, unaleta habari njema. 43 Naye Yonathani akajibu, akamwambia Adonia, Hakika bwana wetu mfalme Daudi amemtawaza Sulemani. 44 Tena mfalme alipeleka pamoja naye Sadoki, kuhani, na Nathani, nabii, na Benaya, mwana wa Yehoyada, na Wakerethi, na Wapelethi, wakampandisha juu ya nyumbu wa mfalme. 45 Kisha Sadoki, kuhani, na Nathani, nabii, wakamtia mafuta huko Gihoni, ili awe mfalme. Nao wamepanda juu kutoka huko wakifurahi, hata mji ukavuma. Ndizo kelele zile mlizozisikia. 46 Na tena, Sulemani ameketi katika kiti cha enzi cha ufalme. 47 Na tena, watumishi wa mfalme walifika, ili wambariki bwana wetu mfalme Daudi, wakisema, Mungu wako na alikuze jina la Sulemani kuliko jina lako, na kukifanya kiti chake cha enzi kuwa kitukufu kuliko kiti chako. Naye mfalme akainama chini juu ya kitanda chake. 48 Na tena, mfalme akasema hivi, Bwana, Mungu wa Israeli, ahimidiwe, aliyenipa leo hivi mtu wa kuketi katika kiti changu cha enzi, nayo macho yangu yakiwa yanaona hayo. 49 Ndipo wageni wote waliokuwa pamoja na Adonia wakaogopa, wakaondoka, wakaenda zao kila mtu njia yake. 50 Adonia naye akaogopa mbele ya Sulemani; akaondoka, akaenda, akazishika pembe za madhabahu. 51 Akaambiwa Sulemani, kusema, Tazama, Adonia amwogopa mfalme Sulemani; kwani, tazama, amezishika pembe za madhabahu, akisema, Mfalme Sulemani na aniapie leo kwamba hataniua mimi mtumwa wake kwa upanga. 52 Akasema Sulemani, Akionekana kuwa mtu wa kweli, hata unywele mmoja wake hautaanguka chini; lakini uovu ukionekana ndani yake, atakufa. 53 Basi mfalme Sulemani akatuma watu, wakamtelemsha toka madhabahuni. Naye akaja, akamwinamia mfalme Sulemani; naye Sulemani akamwambia, Enenda nyumbani kwako.

1 Wafalme 2

1 Basi siku ya kufa kwake Daudi ikakaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, 2 Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; 3 uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako; 4 ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakienda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema), hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli. 5 Na zaidi ya hayo, umejua alivyonitenda Yoabu, mwana wa Seruya, yaani, alivyowatenda majemadari wawili wa majeshi ya Israeli, Abneri, mwana wa Neri, na Amasa, mwana wa Yetheri, ambao aliwaua, na kuimwaga damu ya vita wakati wa amani, akautia damu ya vita mshipi uliokuwa viunoni mwake, na viatu vilivyokuwa miguuni mwake. 6 Kwa hiyo ufanye kama ilivyo hekima yako, wala usimwachie mvi zake kushukia Ahera kwa amani. 7 Lakini uwafanyie mema wana wa Barzilai Mgileadi, wawe miongoni mwao walao mezani pako; kwa jinsi walivyonijilia nilipokuwa nimekimbia mbele ya Absalomu, ndugu yako. 8 Hata, angalia, yuko pamoja nawe Shimei, mwana wa Gera, Mbenyamini, wa Bahurimu, ndiye aliyenilaani kwa laana kuu siku ile nilipokwenda Mahanaimu; lakini akashuka kunilaki kule Yordani, nami nikamwapia kwa Bwana, nikamwambia, Mimi sitakuua kwa upanga. 9 Basi kwa hiyo usimwachilie, kwa kuwa wewe u mtu wa akili; nawe utajua ikupasayo umtendee, na mvi zake utazishusha Ahera pamoja na damu. 10 Basi Daudi akalala na babaze, akazikwa mjini mwa Daudi. 11 Na siku alizotawala Daudi juu ya Israeli zilikuwa miaka arobaini; huko Hebroni alitawala miaka saba, na katika Yerusalemu akatawala miaka thelathini na mitatu. 12 Basi Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha Daudi baba yake; na ufalme wake ukawa imara sana. 13 Ndipo Adonia mwana wa Hagithi akaja kwa Bath-sheba mamaye Sulemani. Naye akasema, Je! Umekuja kwa amani? 14 Naye akajibu, Kwa amani. Tena akasema, Nina shauri ninalotaka kukuambia. Naye akamwambia, Sema. 15 Basi akasema, Wajua ya kwamba ufalme ulikuwa wangu, na Israeli wote wakaniwekea nyuso zao ili nimiliki mimi; walakini sasa ufalme umegeuka kuwa wake ndugu yangu; kwa maana ulikuwa wake kutoka kwa Bwana. 16 Basi sasa nina haja moja ninayokuomba, usinikataze hiyo. Naye akamwambia, Sema. 17 Akasema, Nena, nakusihi, na Sulemani, mfalme, (kwa kuwa hawezi kukukataza neno), kwamba anioze Abishagi, Mshunami. 18 Naye Bath-sheba akasema, Vema; nitasema na mfalme kwa ajili yako. 19 Basi Bath-sheba akaingia kwa mfalme Sulemani, aseme naye kwa ajili ya Adonia. Naye mfalme akainuka kwenda kumlaki, akamwinamia, akaketi katika kiti chake cha enzi; kisha akaagiza awekewe kiti cha enzi mamaye mfalme; naye akaketi mkono wake wa kuume. 20 Ndipo akasema, Haja moja ndogo nakuomba; usinikataze. Mfalme akamwambia, Omba, mama; kwa kuwa siwezi kukukataza neno. 21 Naye akasema, Nataka Adonia, ndugu yako, aozwe Abishagi, Mshunami. 22 Akajibu mfalme Sulemani akamwambia mamaye, Na mbona wamtakia Adonia Abishagi, Mshunami? Umtakie na ufalme pia; kwa kuwa yeye ni ndugu yangu mkubwa; naam, umtakie yeye, na Abiathari kuhani, na Yoabu mwana wa Seruya. 23 Ndipo mfalme Sulemani akaapa kwa Bwana, akasema, Mungu anifanyie hivyo, na kuzidi, isipokuwa Adonia amenena neno hili juu ya uhai wake mwenyewe. 24 Basi kwa hiyo, Bwana aishivyo, aliyenithibitisha na kunikalisha katika kiti cha enzi cha Daudi baba yangu, akanifanyia nyumba, kama alivyoahidi, hakika atauawa leo hivi Adonia. 25 Mfalme Sulemani akatuma kwa mkono wa Benaya mwana wa Yehoyada: naye akampiga, hata akafa. 26 Tena, mfalme akamwambia Abiathari kuhani, Enenda Anathothi mashambani kwako; kwa kuwa wastahili kufa; ila leo sikuui, kwa sababu wewe ulichukua sanduku la Bwana mbele ya Daudi baba yangu, na kwa sababu wewe uliteswa kwa mateso yote ya baba yangu. 27 Hivyo Sulemani akamtoa Abiathari asiwe kuhani wa Bwana; ili alitimize neno la Bwana, alilonena juu ya nyumba ya Eli katika Shilo. 28 Tena, habari zikamfikia Yoabu; kwa maana Yoabu alikuwa amemfuata Adonia, ingawa hakumfuata Absalomu. Yoabu akakimbilia Hemani kwa Bwana, akazishika pembe za madhabahu. 29 Akaambiwa mfalme Sulemani ya kwamba, Yoabu amekimbilia Hemani kwa Bwana, naye, tazama, yuko madhabahuni. Ndipo Sulemani akamtuma Benaya, mwana wa Yehoyada, akisema, Enenda, umpige. 30 Basi Benaya akaja Hemani kwa Bwana, akamwambia, Mfalme asema hivi, Njoo utoke. Naye akajibu, La, sivyo; ila nitakufa papa hapa. Naye Benaya akamletea mfalme habari, akisema, Hivi ndivyo alivyonena Yoabu, na ndivyo alivyonijibu. 31 Mfalme akamwambia, Fanya alivyonena, umpige, ukamzike; ili uniondolee mimi na nyumba ya babangu damu aliyoimwaga Yoabu bure. 32 Naye Bwana atamrudishia damu yake kichwani pake mwenyewe, kwa kuwa aliwapiga watu wawili wenye haki, na wema kuliko yeye, akawaua kwa upanga, wala babangu Daudi hakujua habari hiyo; yaani Abneri, mwana wa Neri, jemadari wa jeshi la Israeli, na Amasa, mwana wa Yetheri, jemadari wa jeshi la Yuda. 33 Hivyo damu yao itarudi kichwani pa Yoabu, na kichwani pa wazao wake hata milele; ila kwa Daudi, na kwa wazao wake, na kwa nyumba yake, na kwa kiti chake cha enzi, kutakuwa na amani hata milele kutoka kwa Bwana. 34 Ndipo Benaya, mwana wa Yehoyada, akapanda, akampiga, akamwua; naye akazikwa katika nyumba yake mwenyewe iliyoko nyikani. 35 Kisha mfalme akamweka Benaya, mwana wa Yehoyada, mahali pake juu ya jeshi; na Sadoki, kuhani, mfalme akamweka mahali pa Abiathari. 36 Tena, mfalme akatuma watu akamwita Shimei, akamwambia, Ujijengee nyumba humu Yerusalemu, ukae ndani yake, wala usitoke humo kwenda mahali po pote. 37 Kwa kuwa siku ile ya kutoka kwako, na kuvuka kijito Kidroni, ujue hakika ya kwamba kufa utakufa; damu yako itakuwa juu ya kichwa chako mwenyewe. 38 Naye Shimei akamwambia mfalme, Neno hili ni jema; kama alivyosema bwana wangu mfalme, ndivyo atakavyofanya mtumwa wako. Basi Shimei akakaa Yerusalemu siku nyingi. 39 Ikawa miaka mitatu ilipokwisha, watumwa wawili wa Shimei wakatoroka kwenda kwa Akishi, mwana wa Maaka, mfalme wa Gathi. Wakamwambia Shimei, wakasema, Angalia, watumwa wako wako huko Gathi. 40 Shimei akaondoka, akatandika punda wake, akaenda Gathi kwa Akishi, ili kuwatafuta watumwa wake. Akaenda Shimei, akawaleta watumwa wake toka Gathi. 41 Naye Sulemani akaambiwa, ya kwamba Shimei alikuwa ametoka Yerusalemu kwenda Gathi, na kurudi tena. 42 Basi, mfalme akatuma watu, akamwita Shimei, akamwambia, Je! Sikukuapisha kwa Bwana, na kukushuhudia, kusema, Siku ile ya kutoka kwako ukienda mahali po pote, ujue hakika ya kwamba kufa utakufa? Nawe ukaniambia, Neno hili nililolisikia ni jema? 43 Mbona basi hukukishika kiapo cha Bwana, na amri niliyokuagiza? 44 Tena, mfalme akamwambia Shimei, Umejua uovu wote uliouona moyoni mwako, uliomtenda Daudi baba yangu; basi kwa hiyo Bwana atakurudishia uovu wako kichwani pako mwenyewe. 45 Ila mfalme Sulemani atakuwa amebarikiwa, na kiti cha enzi cha Daudi kitathibitika mbele za Bwana hata milele. 46 Basi mfalme akamwamuru Benaya, mwana wa Yehoyada; naye akatoka, akampiga, hata akafa. Nao ufalme ukawa imara mkononi mwa Sulemani.

1 Wafalme 3

1 Huyo Sulemani akafanya ujamaa na Farao, mfalme wa Misri, akamwoa binti yake Farao, akamleta mjini mwa Daudi, hata alipokwisha kuijenga nyumba yake, na nyumba ya Bwana, na ukuta wa kuuzunguka Yerusalemu. 2 Ila watu walikuwa wakichinja dhabihu katika mahali pa juu, kwa sababu haikuwapo nyumba iliyojengwa kwa jina la Bwana, hata siku zile. 3 Sulemani naye akampenda Bwana, akienda katika amri za Daudi babaye, ila hutoa dhabihu na kufukiza uvumba katika mahali pa juu. 4 Basi mfalme akaenda Gibeoni, ili atoe dhabihu huko; kwa kuwa ndipo mahali pa juu palipo pakuu. Sulemani akatoa sadaka elfu za kuteketezwa juu ya madhabahu ile. 5 Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. 6 Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo. 7 Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. 8 Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. 9 Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? 10 Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. 11 Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; 12 basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe. 13 Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote. 14 Nawe ukienda katika njia zangu, na kuyashika mausia yangu, na amri zangu, kama baba yako Daudi alivyokwenda, basi nitazifanya siku zako kuwa nyingi. 15 Naye Sulemani akaamka, na kumbe! Ni ndoto. Akaenda Yerusalemu, akasimama mbele ya sanduku la agano la Bwana, akatoa sadaka za kuteketezwa, akatoa na sadaka za amani; akawafanyia karamu watumishi wake wote. 16 Ndipo wanawake wawili, makahaba, walimwendea mfalme, wakasimama mbele yake. 17 Na mwanamke mmoja akasema, Ee bwana wangu, mimi na mwanamke huyu tunakaa katika nyumba moja; nami nalizaa nilipokuwa pamoja naye nyumbani. 18 Kisha, siku ya tatu baada ya kuzaa kwangu, ikawa mwanamke huyu naye akazaa; na sisi tulikuwa pamoja; hapakuwa na mtu mwingine pamoja nasi nyumbani, isipokuwa sisi wawili tu. 19 Na mtoto wa mwanamke huyu akafa usiku, maana alimlalia. 20 Akaondoka kati ya usiku, akamwondoa mtoto wangu ubavuni pangu, mimi mjakazi wako nilipokuwa usingizini, akamweka kifuani pake, na mtoto wake mwenyewe, aliyekuwa amekufa, akamweka kifuani pangu. 21 Nilipoondoka asubuhi nimnyonyeshe mtoto wangu, kumbe? Amekufa. Hata asubuhi nilipomtazama sana, kumbe! Siye mtoto wangu niliyemzaa. 22 Ndipo yule mwanamke wa pili akasema, Sivyo hivyo; bali mtoto wangu ndiye aliye hai, na mtoto wako ndiye aliyekufa. Na mwenzake akasema, Sivyo hivyo; bali mtoto wako ndiye aliyekufa, na mtoto wangu ndiye aliye hai. Ndivyo walivyosema mbele ya mfalme. 23 Ndipo mfalme akasema, Huyu anasema, Mtoto wangu yu hai, na mtoto wako amekufa. Na huyu anasema, Sivyo hivyo; bali mtoto aliyekufa ni wako, na mtoto aliye hai ni wangu. 24 Mfalme akasema, Nileteeni upanga. Wakaleta upanga mbele ya mfalme. 25 Mfalme akasema, Mkate mtoto aliye hai vipande viwili, kampe huyu nusu, na huyu nusu. 26 Ndipo mwanamke yule, ambaye mtoto aliye hai ni wake, akamwambia mfalme kwa maana moyoni mwake alimwonea mtoto wake huruma, akasema, Ee bwana wangu, mpe huyu mtoto aliye hai, wala usimwue kamwe. Lakini yule mwingine akasema, Asiwe wangu wala wako; na akatwe. 27 Ndipo mfalme akajibu, akasema, Mpe huyu wa kwanza mtoto aliye hai, maana yeye ndiye mama yake. 28 Na Israeli wote wakapata habari za hukumu ile aliyoihukumu mfalme wakamwogopa mfalme; maana waliona ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake, ili afanye hukumu.

1 Wafalme 4

1 Basi mfalme Sulemani akawa mfalme juu ya Israeli wote. 2 Na hawa ndio wakuu aliokuwa nao; Azaria mwana wa Sadoki, kuhani, 3 Elihorefu na Ahiya, wana wa Shausha, waandishi; Yehoshafati mwana wa Ahiludi mwenye kuandika tarehe; 4 na Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa juu ya jeshi; na Sadoki na Abiathari walikuwa makuhani; 5 na Azaria mwana wa Nathani alikuwa juu ya maakida; na Zabudi mwana wa Nathani alikuwa kuhani, rafiki wake mfalme. 6 Na Ahishari alikuwa juu ya nyumba; na Adoramu mwana wa Abda alikuwa juu ya shokoa. 7 Sulemani alikuwa na maakida kumi na wawili juu ya Israeli wote, walioleta chakula cha mfalme na nyumba yake; kila mtu alikuwa na mwezi mmoja katika mwaka kuleta chakula. 8 Na haya ndiyo majina yao. Mwana wa Huri, mlimani mwa Efraimu. 9 Mwana wa Dekari, kutoka Makasi, na Shaalbimu na Bethshemeshi na Elon-beth-hanani. 10 Mwana wa Hesedi, katika Arubothi; na Soko ilikuwa kwake na nchi yote ya Heferi. 11 Mwana wa Abinadabu katika Nafath-dori yote; ndiye aliyekuwa naye Tafathi binti Sulemani kuwa mke wake. 12 Baana mwana wa Ahiludi, katika Taanaki na Megido, na Beth-sheani yote, iliyo kando ya Sarethani, chini ya Yezreeli, tangu Beth-sheani mpaka Abel-mehola, hata kupita Yokmeamu. 13 Mwana wa Geberi katika Ramoth-gileadi; na kwake ilikuwa miji ya Yairi mwana wa Manase iliyomo Gileadi; na kwake ilikuwa wilaya ya Argobu, iliyomo Bashani, miji mikubwa sitini yenye kuta na makomeo ya shaba. 14 Ahinadabu mwana wa Ido, katika Mahanaimu. 15 Ahimaasi, katika Naftali; naye ndiye aliyemwoa Basemathi binti Sulemani. 16 Baana mwana wa Hushai, katika Asheri na Bealothi. 17 Yehoshafati mwana wa Parua, katika Isakari. 18 Shimei mwana wa Ela, katika Benyamini. 19 Geberi mwana wa Uri, katika nchi ya Gileadi, nchi ya Sihoni mfalme wa Waamori, na Ogu mfalme wa Bashani; naye alikuwa akida wa pekee katika nchi hiyo. 20 Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi. 21 Sulemani akatawala juu ya falme zote, toka Mto mpaka nchi ya Wafilisti, na hata mpaka wa Misri; walimletea tunu, na kumtumikia Sulemani siku zote za maisha yake. 22 Na vyakula vya Sulemani vya siku moja vilikuwa kori therathini za unga wa mzuri, na kori sitini za ngano. 23 na ng'ombe kumi walionona, na ng'ombe ishirini za malisho, na kondoo mia, pamoja na ayala, na paa, na kulungu, na kuku walionona. 24 Kwani alikuwa akitawala nchi yote upande huu wa Mto, toka Tifsa mpaka Gaza, juu ya wafalme wote wa upande huu wa Mto; naye alikuwa na amani pande zake zote. 25 Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani. 26 Tena Sulemani alikuwa na mabanda ya farasi arobaini elfu kwa magari yake, na wapandao farasi kumi na mbili elfu. 27 Na maakida wale wakaleta chakula kwa mfalme Sulemani na kwa wote walioijia meza ya mfalme Sulemani, kila mtu katika mwezi wake, kisipunguke kitu. 28 Shayiri pia na majani kwa farasi, na kwa wanyama wenye mbio, wakaleta mahali walipokuwapo, kila mtu kwa kadiri ya kazi yake. 29 Mungu akampa Sulemani hekima, na akili nyingi sana, na moyo mkuu, kama mchanga ulioko pwani. 30 Hekima ya Sulemani ikapita hekima ya wana wote wa mashariki, na hekima zote za Misri. 31 Kwa kuwa alikuwa na hekima kuliko watu wote; kuliko Ethani Mwezrahi, na Hemani, na Kalkoli, na Darda, wana wa Maholi; zikaenea sifa zake kati ya mataifa yote yaliyozunguka. 32 Naye akanena mifano elfu tatu, na nyimbo zake zilikuwa elfu moja na tano. 33 Akanena habari za miti tangu mwerezi ulioko Lebanoni hata hisopo umeao ukutani; pia akanena habari za wanyama, na za ndege, na vitambaavyo, na samaki. 34 Wakaja wa mataifa yote ili waisikie hekima ya Sulemani, toka wafalme wote wa ulimwengu, waliokuwa wamepata habari za hekima yake.

1 Wafalme 5

1 Ndipo Hiramu, mfalme wa Tiro, akawatuma watumishi wake kwa Sulemani; kwani alikuwa amesikia ya kwamba wamemtia mafuta awe mfalme mahali pa baba yake. Kwa maana Hiramu alikuwa akimpenda Daudi siku zote. 2 Basi Sulemani akatuma watu kwa Hiramu, akasema, 3 Umemjua Daudi baba yangu jinsi asivyoweza kujenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wake, kwa sababu ya vita vilivyomzunguka pande zote, hata Bwana alipowatia watu chini ya nyayo zake. 4 Ila leo Bwana, Mungu wangu, amenipa amani kila upande; hakuna adui, wala tukio baya. 5 Nami, tazama, nakusudia kujenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wangu, kama Bwana alivyomwambia Daudi baba yangu, akisema, Mwana wako, nitakayemweka katika kiti chake cha enzi mahali pako, ndiye atakayeijenga nyumba kwa jina langu. 6 Basi uamuru wanikatie mierezi ya Lebanoni; na watumishi wangu watafuatana na watumishi wako; na ujira wa watumishi wako nitakupa kama utakavyosema; kwa kuwa wajua ya kwamba hakuna kwetu mtu ajuaye kukata miti kama Wasidoni. 7 Ikawa, Hiramu aliposikia maneno yake Sulemani, alifurahi sana, akasema, Na ahimidiwe Bwana leo, aliyempa Daudi mwana mwenye akili juu ya watu hawa walio wengi. 8 Hiramu akatuma watu kwa Sulemani, akasema, Nimeyasikia yale uliyoniletea; nami nitafanya kila ulitakalo katika habari ya miti ya mierezi, na miti ya miberoshi. 9 Watumishi wangu wataishusha toka Lebanoni mpaka baharini; nami nitaiendesha baharini, ikifungwa pamoja, mpaka mahali utakaponiagiza, huko nitaifungua ili wewe uichukue; ndivyo utakavyoitimiza haja yangu, ukiwapa chakula watu wa nyumbani mwangu. 10 Basi Hiramu akampa Sulemani miti ya mierezi na miti ya miberoshi kadiri alivyotaka. 11 Sulemani akampa Hiramu kori ishirini elfu za ngano, chakula cha watu wake, na kori ishirini za mafuta safi. Ndizo Sulemani alizompa Hiramu mwaka kwa mwaka. 12 Bwana akampa Sulemani hekima, kama alivyomwahidia. Ikawa amani kati yao Hiramu na Sulemani; wakafanyana maagano pamoja hao wawili. 13 Mfalme Sulemani akafanya shokoa ya Israeli wote; nayo shokoa hiyo ilikuwa ya watu thelathini elfu. 14 Akawatuma Lebanoni kwa mwezi, elfu kumi kwa zamu. Mwezi mmoja walikuwako huko Lebanoni, na miezi miwili wakawako kwao. Na Adoramu alikuwa juu ya shokoa. 15 Sulemani alikuwa na wachukua mizigo sabini elfu, na wakatao miti themanini elfu milimani; 16 mbali na maakida yake Sulemani waliokuwa juu ya kazi, elfu tatu na mia tatu, wasimamizi wa watu waliotenda kazi. 17 Mfalme akaamuru, nao wakaleta mawe makubwa, mawe ya thamani, ili wauweke msingi wa nyumba kwa mawe yaliyochongwa. 18 Na waashi wa Sulemani na waashi wa Hiramu na Wagebali wakayachonga, wakaweka tayari miti na mawe ya kuijenga nyumba.

1 Wafalme 6

1 Ikawa katika mwaka wa mia nne na themanini baada ya kutoka wana wa Israeli katika nchi ya Misri, katika mwaka wa nne wa kutawala kwake Sulemani juu ya Israeli, katika mwezi wa Zivu, ndio mwezi wa pili, akaanza kuijenga nyumba ya Bwana. 2 Nayo nyumba hiyo mfalme Sulemani aliyomjengea Bwana, urefu wake ulikuwa mikono sitini, na upana wake ishirini, na kwenda juu kwake mikono thelathini. 3 Na ukumbi mbele ya hekalu la nyumba, urefu wake ulikuwa mikono ishirini, kadiri ya upana wa nyumba; na upana wake mikono kumi mbele ya nyumba. 4 Akaifanyia nyumba madirisha ya miangaza yenye kimia. 5 Nao ukuta wa nyumba akauzungushia vyumba, kushikamana na kuta za nyumba kote kote, za hekalu na za chumba cha ndani; akafanya vyumba vya mbavuni pande zote. 6 Chumba cha chini kilikuwa mikono mitano upana wake, na chumba cha katikati kilikuwa mikono sita upana wake, na chumba cha tatu kilikuwa mikono saba upana wake; kwa kuwa upande wa nje akaupunguza ukuta wa nyumba pande zote, ili boriti zisishikamane kutani mwa nyumba. 7 Na nyumba ilipokuwa ikijengwa, ikajengwa kwa mawe yaliokwisha kuchongwa chimboni; wala nyundo, wala shoka, wala chombo cha chuma cho chote, sauti yake haikusikiwa ilipokuwa ikijengwa nyumba. 8 Mlango wa vyumba vya chini ulikuwapo upande wa kuume wa nyumba; mtu hupanda madaraja ya kuzunguka mpaka vyumba vya katikati, na kutoka vile vya katikati mpaka vile vya tatu. 9 Basi ndivyo alivyoijenga nyumba, akaimaliza; akaifunika nyumba kwa boriti na mbao za mwerezi. 10 Akavijenga vyumba mbavuni mwa nyumba yote, kwenda juu kwake kila kimoja kilikuwa mikono mitano; vikaitegemea nyumba kwa boriti za mwerezi. 11 Neno la Bwana likamjia Sulemani, kusema, 12 Katika habari ya nyumba hii unayoijenga, kama ukienda katika sheria zangu, na kuzifanya hukumu zangu, na kuzishika amri zangu zote na kwenda katika hizo; ndipo nitakapolithibitisha neno langu kwako, nililomwambia Daudi baba yako. 13 Nami nitakaa katikati ya wana wa Israeli, wala sitawaacha watu wangu Israeli. 14 Basi Sulemani akaijenga hiyo nyumba akaimaliza. 15 Akazijenga kuta za nyumba ndani kwa mbao za mwerezi; toka sakafu ya nyumba hata boriti za juu, akazifunika ndani kwa mti; akafunika sakafu ya nyumba kwa mbao za mberoshi. 16 Akajenga mikono ishirini pande za nyuma za nyumba toka chini hata juu kwa mbao za mwerezi; naam, ndani akaijengea chumba cha ndani, yaani, patakatifu pa patakatifu. 17 Nayo nyumba, ndiyo hekalu la mbele, ilikuwa mikono arobaini. 18 Na ndani ya nyumba, mlikuwa na mwerezi ulionakishiwa maboga na maua yaliyofunuka wazi; mlikuwa na mwerezi mahali pote; wala mawe hayakuonekana. 19 Akaweka tayari chumba cha ndani katikati ya nyumba ndani, ili atie humo sanduku la agano la Bwana. 20 Na ndani yake chumba hicho cha ndani mlikuwa na nafasi, mikono ishirini urefu, na mikono ishirini upana, na mikono ishirini kwenda juu kwake; akaifunika na dhahabu safi. Akaifunika madhabahu nayo kwa mwerezi. 21 Hivyo Sulemani akaifunika nyumba ndani kwa dhahabu safi. Akaitenga kwa mikufu ya dhahabu mbele ya chumba cha ndani; akapafunika na dhahabu. 22 Akaifunika nyumba yote kwa dhahabu, hata ilipokwisha nyumba yote; tena madhabahu yote iliyokuwa ya chumba cha ndani akaifunika kwa dhahabu. 23 Akafanya ndani ya chumba cha ndani makerubi mawili ya mzeituni, kwenda juu mikono kumi. 24 Na bawa moja la kerubi lilikuwa mikono mitano urefu wake, na bawa la pili la kerubi mikono mitano; mikono kumi toka mwisho wa bawa moja hata mwisho wa bawa la pili. 25 Na kerubi la pili lilikuwa mikono kumi; makerubi yote mawili walikuwa ya cheo kimoja na namna moja. 26 Kwenda juu kwake kerubi moja kulikuwa mikono kumi, na kerubi la pili vivyo. 27 Akayaweka hayo makerubi katika nyumba ya ndani; na mabawa ya makerubi yakanyoshwa, bawa la moja likafika ukutani huko, na bawa la kerubi la pili likafika ukutani huko; mabawa yao yakagusana katikati ya nyumba. 28 Akayafunika makerubi kwa dhahabu. 29 Akazinakshi kuta zote za nyumba kwa nakshi za makerubi, na mitende, na maua yaliyofunuka wazi, pande za ndani na nje. 30 Na sakafu ya nyumba akaifunika na dhahabu ndani na nje. 31 Akayafanyia maingilio ya chumba cha ndani milango ya mzeituni; kizingiti na miimo ilikuwa ya pande tano. 32 Hivyo akafanya milango miwili ya mzeituni; akanakshi juu yake nakshi za makerubi, na mitende, na maua yaliyofunuka wazi, akaifunika kwa dhahabu; akatia dhahabu juu ya makerubi, na juu ya mitende. 33 Ndivyo alivyoyafanyia maingilio ya hekalu miimo ya mzeituni, yenye pande nne; 34 na milango miwili ya mberoshi; mbao mbili za mlango mmoja zilikuwa za kukunjana, na mbao mbili za mlango wa pili za kukunjana. 35 Akanakshi juu yake makerubi, na mitende, na maua yaliyofunuka wazi; akazifunika kwa dhahabu iliyonyoshwa juu ya machoro. 36 Akaijengea behewa ya ndani safu tatu za mawe ya kuchongwa, na safu moja ya mihimili ya mierezi. 37 Katika mwaka wa nne nyumba ya Bwana ilitiwa msingi, katika mwezi wa Zivu. 38 Hata katika mwaka wa kumi na mmoja, katika mwezi wa Buli, ndio mwezi wa nane, nyumba ikaisha, mambo yake yote, na sharti zake zote. Basi muda wa miaka saba alikuwa katika kuijenga.

1 Wafalme 7

1 Naye Sulemani alikuwa katika kuijenga nyumba yake mwenyewe miaka kumi na mitatu, akaimaliza nyumba yake yote. 2 Kwa kuwa aliijenga nyumba ya mwitu wa Lebanoni; mikono mia urefu wake, na mikono hamsini upana wake, na mikono thelathini kwenda juu kwake, juu ya safu nne za nguzo za mwerezi, na mihimili ya mwerezi juu ya nguzo. 3 Ikafunikwa juu kwa mwerezi juu ya mihimili arobaini na mitano, iliyokuwa juu ya nguzo; kumi na mitano kwa safu. 4 Na madirisha yalikuwako safu tatu, mwangaza kuelekea mwangaza katika madaraja matatu. 5 Na milango yote na miimo ilikuwa ya mraba, ilivyoangaziwa; na mwangaza kuelekea mwangaza katika madaraja matatu. 6 Akaifanya baraza ya nguzo; mikono hamsini urefu wake, na mikono thelathini upana wake; na ukumbi mbele yake; na nguzo na mihimili minene mbele yake. 7 Akaifanya baraza ya kiti cha enzi, ili ahukumu ndani yake, ndiyo baraza ya hukumu; nayo ikafunikwa mwerezi tangu sakafu mpaka dari. 8 Nayo nyumba yake atakayokalia, katika behewa nyingine iliyokuwa ndani kupita baraza, ilikuwa ya kazi kama hiyo. Tena akamjengea nyumba binti Farao, (ambaye Sulemani alikuwa amemwoa), mfano wa ile baraza. 9 Hizi zote zilikuwa za mawe ya thamani, mawe ya kuchongwa, sawasawa na cheo, yaliyokatwa kwa misumeno, ndani na nje, tangu msingi hata mawe ya juu, na nje vile vile hata behewa kuu. 10 Nao msingi ulikuwa wa mawe ya thamani, mawe makubwa, mawe mikono kumi, na mawe ya mikono minane. 11 Na juu kulikuwa na mawe ya thamani, mawe ya kuchongwa, sawasawa na cheo, na mierezi. 12 Na behewa kubwa pande zote ilikuwa na safu tatu za mawe ya kuchongwa, na safu moja ya mihimili ya mierezi; mfano wa behewa ya ndani ya nyumba ya Bwana, na ukumbi wa nyumba. 13 Mfalme Sulemani akatuma watu kumleta Huramu kutoka Tiro. 14 Naye alikuwa mwana wa mwanamke mjane wa kabila ya Naftali, na babaye alikuwa mtu wa Tiro, mfua shaba; naye alikuwa mwingi wa hekima na akili, mstadi wa kufanya kazi zote za shaba. Akamfikilia mfalme Sulemani, akamfanyia kazi yake yote. 15 Kwa maana alizifanyiza zile nguzo mbili za shaba, mikono kumi na minane kwenda juu kwake kila moja; na uzi wa mikono kumi na miwili kuizunguka nguzo hii au hii. 16 Akafanya taji mbili za shaba iliyoyeyushwa za kuwekwa juu ya vichwa vya nguzo; kwenda juu kwake taji moja mikono mitano, na mikono mitano kwenda juu kwake taji ya pili. 17 Kulikuwa na nyavu kama kazi ya kusuka, na masongo ya mikufu, kwa taji zilizokuwako juu ya vichwa vya nguzo; saba kwa taji moja, na saba kwa taji ya pili 18 Hivyo akazifanya nguzo; na kulikuwa na safu mbili za kuzunguka juu ya wavu mmoja, zifunike taji zilizokuwako juu ya vichwa vya nguzo; akafanya vivyo hivyo kwa taji ya pili. 19 Na taji zilizokuwa juu ya nguzo ukumbini zilikuwa za kazi ya mayungi, mikono minne. 20 Kulikuwako tena taji juu ya nguzo mbili, karibu na uvimbe uliokuwako kando ya wavu; na makomamanga yalikuwa mia mbili, safu safu pande zote juu ya taji ya pili. 21 Akazisimamisha nguzo ukumbini pa hekalu; akaisimamisha nguzo ya kuume, akaiita jina lake Yakini; akaisimamisha nguzo ya kushoto ,akaiita jina lake Boazi. 22 Na juu ya nguzo kulikuwa na kazi ya mayungi; hivyo mambo ya nguzo yakatimia. 23 Tena akaifanya bahari ya kusubu, mikono kumi toka ukingo hata ukingo, ikaviringana, na mikono mitano ilikuwa kwenda juu kwake; na uzi wa mikono thelathini kuizunguka kabisa. 24 Na chini ya ukingo wake kulikuwa na maboga yaliyoizunguka, kwa mikono kumi, yakiizunguka bahari; kulikuwa na safu mbili za hayo maboga, yakafanywa kalibuni hapo bahari ilipofanywa. 25 Ikakaa juu ya ng'ombe kumi na wawili, watatu wakitazama kaskazini, na watatu wakitazama magharibi, na watatu wakitazama kusini, na watatu wakitazama mashariki; na bahari iliwekwa juu yao, na pande zao za nyuma zote zilikuwa ndani. 26 Na unene wake ulikuwa nyanda nne; na ukingo wake ukafanywa kama ukingo wa kikombe, kama ua la yungi; huingia bathi elfu mbili. 27 Akayafanya yale matako kumi ya shaba; mikono minne urefu wa tako moja, na mikono minne upana wake, na mikono mitatu kwenda juu kwake. 28 Na kazi ya matako ndiyo hii; yalikuwa na papi; na papi zilikuwa katikati ya vipandio; 29 na juu ya papi zilizokuwa katikati ya vipandio kulikuwa na simba, na ng'ombe, na makerubi; na juu ya vipandio kulikuwa na tako; na chini ya simba na ng'ombe kulikuwa na masongo ya kazi ya kupembeza. 30 Kila tako lilikuwa na magurudumu manne ya shaba, na vipini vya shaba; na miguu yake minne ilikuwa na mataruma; chini ya birika yalikuwako mataruma ya kusubu, yenye masongo kila moja mbavuni. 31 Na kinywa chake ndani ya taji na juu yake kilikuwa mkono mmoja; na kinywa chake kikaviringana kama kazi ya tako, mkono mmoja na nusu; tena juu ya kinywa chake kulikuwa na nakshi, na papi zao zilikuwa za mraba, wala hazikuviringana. 32 Na magurudumu manne yalikuwa chini ya papi; na mikono ya magurudumu ndani ya tako; na kwenda juu kwake gurudumu moja mkono mmoja na nusu. 33 Na kazi ya magurudumu ilikuwa kama kazi ya gurudumu la gari; mikono yake, na maduara, na matindi, na vipande vya ndani, vyote vilikuwa vya kusubu. 34 Kulikuwa na mataruma manne katika pembe nne za tako moja; mataruma hayo ni kitu kimoja na tako lenyewe. 35 Na juu ya tako kulikuwa na duara nusu mkono kwenda juu kwake; na juu ya tako mashikio yake na papi zake vilikuwa vya namna iyo hiyo. 36 Akachora juu ya mabamba ya mashikio yake, na juu ya papi zake, makerubi, na simba, na mitende, moja moja kama ilivyokuwa nafasi, na masongo pande zote. 37 Hivyo akayafanya yale matako kumi; yote yalikuwa ya kalibu moja, na cheo kimoja, na namna moja. 38 Akafanya birika kumi za shaba; birika moja huingia bathi arobaini; na kila birika ilikuwa mikono minne; birika moja juu ya tako moja, katika yale matako kumi. 39 Akayaweka yale matako, matano upande wa kuume wa nyumba, na matano upande wa kushoto wa nyumba; akaiweka ile bahari upande wa kuume wa nyumba upande wa mashariki, kuelekea kusini. 40 Tena Huramu akazifanya birika, na majembe, na mabakuli. Hivyo Huramu akazimaliza kazi zote alizomfanyia mfalme Sulemani katika nyumba ya Bwana; 41 zile nguzo mbili, na vimbe mbili za taji zilikuwa juu ya nguzo; na nyavu mbili za kuzifunika hizo vimbe mbili za taji zilizokuwa juu ya nguzo; 42 na makomamanga mia nne ya zile nyavu mbili; safu mbili za makomamanga kwa kila wavu, kuzifunika hizo vimbe mbili za taji zilizokuwa juu ya nguzo; 43 na yale matako kumi, na birika kumi juu ya matako; 44 na ile bahari moja, na ng'ombe kumi na wawili chini ya ile bahari; 45 na masufuria, na majembe, na mabakuli; hata vyombo hivyo vyote, Huramu alivyomfanyia mfalme Sulemani, katika nyumba ya Bwana, vyote vilikuwa vya shaba iliyosuguliwa. 46 Katika uwanda wa Yordani ndipo mfalme alipovisubu, katika udongo mzito kati ya Sukothi na Sarethani. 47 Sulemani akaviacha vyombo vyote visipimwe kwa kuwa vilikuwa vingi mno; wala uzito wa shaba haukujulikana. 48 Sulemani akavifanya vyombo vyote vilivyokuwamo nyumbani mwa Bwana; madhabahu ya dhahabu, na ile meza iliyokuwa na mikate ya wonyesho juu yake ilikuwa ya dhahabu; 49 na vinara vya taa, vitano upande wa kuume, na vitano upande wa kushoto, mbele ya chumba cha ndani, vya dhahabu safi; na maua, na taa, na koleo ya dhahabu; 50 na vikombe, na makasi, na mabakuli, na miiko, na vyetezo, vya dhahabu safi; na bawaba za dhahabu, za milango ya nyumba ya ndani, yaani, patakatifu pa patakatifu, na za milango ya nyumba, ndiyo hekalu. 51 Hivyo ikamalizika kazi yote Sulemani mfalme aliyoifanya katika nyumba ya Bwana. Sulemani akaviingiza vile vitu alivyovitakasa Daudi baba yake, yaani, fedha, na dhahabu, na vyombo; akavitia ndani ya hazina za nyumba ya Bwana.

1 Wafalme 8

1 Ndipo Sulemani alipowakusanya wazee wa Israeli, na wakuu wote wa kabila, wakuu wa mbari za mababa wa wana wa Israeli, wamwendee mfalme Sulemani huko Yerusalemu, ili walipandishe sanduku la agano la Bwana kutoka mji wa Daudi, yaani, Sayuni. 2 Wakakutana mbele ya mfalme Sulemani watu wote wa Israeli wakati wa sikukuu, katika mwezi wa Ethanimu, ndio mwezi wa saba. 3 Wazee wote wa Israeli wakaja, nao makuhani wakajitwika sanduku. 4 Wakalipandisha sanduku la Bwana, na ile hema ya kukutania, na vyombo vitakatifu vyote vilivyokuwa katika ile Hema; vitu hivyo makuhani na Walawi wakavipandisha. 5 Mfalme Sulemani, na mkutano wote wa Israeli waliokutanika kwake, walikuwako pamoja naye mbele ya sanduku, wakichinja sadaka kondoo na ng'ombe, wasioweza kuhesabiwa wala kufahamiwa idadi yao kwa kuwa wengi. 6 Makuhani wakalileta sanduku la agano la Bwana hata mahali pake, katika chumba cha ndani cha ile nyumba, patakatifu pa patakatifu, naam, chini ya mbawa za makerubi. 7 Kwa maana makerubi yalinyosha mbawa zao, juu ya mahali pa sanduku, makerubi yakalifunika lile sanduku na miti yake kwa juu. 8 Na ile miti kwa kuwa mirefu, ncha za miti zilionekana katika mahali patakatifu, mbele ya chumba cha ndani; lakini hazikuonekana nje; nayo iko kuko huko hata leo. 9 Hamkuwa na kitu ndani ya sanduku, ila zile mbao mbili za mawe ambazo Musa aliziweka ndani huko Horebu, Bwana alipofanya agano na wana wa Israeli, hapo walipotoka katika nchi ya Misri. 10 Ikawa, makuhani walipotoka katika patakatifu, nyumba ya Bwana ikajaa wingu; 11 hata makuhani hawakuweza kusimama ili kufanya huduma yao, kwa sababu ya wingu lile; kwa kuwa nyumba ya Bwana ilikuwa imejaa utukufu wa Bwana. 12 Ndipo Sulemani akanena, Bwana alisema ya kwamba atakaa katika giza nene. 13 Hakika nimekujengea nyumba ya kukaa, iwe mahali pa makao yako milele. 14 Mfalme akageuza uso wake, akawabariki mkutano wote wa Israeli; na mkutano wote wa Israeli wakasimama. 15 Akasema, Bwana, Mungu wa Israeli, ahimidiwe, aliyenena na Daudi baba yangu kwa kinywa chake akalitimiza kwa mkono wake, akasema, 16 Tokea siku ile nilipowatoa watu wangu Israeli katika Misri, sikuchagua mji wo wote katika kabila zote za Israeli ili kujenga nyumba, jina langu liwe hapo; lakini nalimchagua Daudi awe juu ya watu wangu Israeli. 17 Basi ilikuwa moyoni mwake Daudi, baba yangu, kujenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wa Israeli. 18 Lakini Bwana akamwambia Daudi baba yangu, Kwa kuwa ilikuwa moyoni mwako kujenga nyumba kwa jina langu, ulifanya vema kuwaza hivi moyoni mwako. 19 Lakini wewe hutanijengea nyumba hiyo; ila mwanao atakayetoka katika viuno vyako, yeye ndiye atakayeijenga nyumba kwa jina langu. 20 Basi Bwana amelitimiza neno lile alilolinena; nami nimesimama mahali pa Daudi baba yangu, na kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli, kama Bwana alivyoahidi, nami nimeijenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wa Israeli. 21 Na humo sanduku hili nimelifanyizia mahali, ambalo ndani yake mna maagano ya Bwana, aliyoyafanya na baba zetu, hapo alipowatoa katika nchi ya Misri. 22 Sulemani akasimama mbele ya madhabahu ya Bwana, machoni pa mkutano wote wa Israeli, akaikunjua mikono yake mbinguni. 23 Akasema Ee Bwana, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe, mbinguni juu wala duniani chini; ushikaye maagano na rehema kwa watumishi wako, waendao mbele zako kwa mioyo yao yote. 24 Umemtimizia mtumishi wako, Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidia; naam, ulinena kwa kinywa chako, ukayatimiza kwa mkono wako, kama ilivyo leo. 25 Na sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, umfikilizie mtumishi wako, Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidia, ukisema, Hutakosa kuwa na mtu wa kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli machoni pangu, kama watoto wako wakiangalia njia zao, ili kuenenda mbele zangu kama wewe ulivyoenenda. 26 Sasa, Ee Mungu wa Israeli, nakusihi, ulithibitishe neno lako, ulilomwambia mtumishi wako, Daudi, baba yangu. 27 Lakini Mungu je? Atakaa kweli kweli juu ya nchi? Tazama, mbingu hazikutoshi, wala mbingu za mbingu; sembuse nyumba hii niliyoijenga! 28 Walakini uyaelekee maombi ya mtumwa wako, na dua yake, Ee Bwana, Mungu wangu, uisikilize sauti na maombi ya mtumwa wako, aombayo mbele zako leo. 29 Macho yako yafumbuke na kuielekea nyumba hii usiku na mchana, mahali hapa ulipopataja, ukasema, Hapa ndipo litakapokuwapo jina langu; ili uyasikie maombi ya mtumwa wako aombapo akikabili mahali hapa. 30 Uisikie dua ya mtumwa wako, na ya watu wako Israeli, watakapoomba wakikabili mahali hapa; naam, sikia huko mbinguni, makao yako; nawe usikiapo, samehe. 31 Ikiwa mtu amemkosa mwenzake, na kupewa sharti ya kiapo aapishwe, naye akija na kuapa hapa mbele ya madhabahu yako, katika nyumba hii; 32 basi, usikie huko mbinguni, ukatende, ukawahukumu watumwa wako; ukimpatiliza mtu mbaya, kwa kuleta njia yake juu ya kichwa chake; na kumpa mwenye haki haki yake, ukimjalia kwa kadiri ya haki yake. 33 Ikiwa watu wako Israeli wamepigwa mbele ya adui zao, kwa sababu wamekukosa wewe; kama wakirejea tena kwako, na kulikiri jina lako wakikuomba na kukusihi katika nyumba hii; 34 basi, usikie huko mbinguni, ukawaachilie watu wako Israeli dhambi yao, ukawarejeze tena katika nchi uliyowapa baba zao. 35 Ikiwa mbingu zimefungwa, hata hakuna mvua, kwa sababu wamekukosa wewe; kama wakiomba wakikabili mahali hapa, na kulikiri jina lako, na kuiacha dhambi yao, wakati ule utakapowatesa; 36 basi, usikie huko mbinguni, ukaisamehe dhambi ya watumwa wako, na ya watu wako Israeli; unapowafundisha njia iliyo njema, iwapasayo kuiendea; ukanyeshe mvua juu ya nchi yako, uliyowapa watu wako iwe urithi wao. 37 Ikiwa nchi imeingia njaa, au tauni, au ukosefu wa mvua, au ukungu, au nzige, au panzi; ikiwa adui wamewahusuru katika nchi ya miji yao; au ukiwapo msiba wo wote, au uele wo wote; 38 maombi yo yote au dua yo yote ikifanywa na mtu awaye yote, au na watu wako Israeli wote pamoja, watakaojua kila mtu maradhi ya moyo wake, na kuikunjua mikono yake kuielekea nyumba hii; 39 basi, usikie huko mbinguni, makao yako, ukasamehe, ukatende, ukampe kila mtu kwa kadiri ya njia zake; wewe ujuaye moyo wake; (maana wewe peke yako ndiwe uijuaye mioyo ya wanadamu wote); 40 ili wakuche wewe siku zote watakazoishi katika nchi uliyowapa baba zetu. 41 Hata na mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako; 42 (maana watasikia habari za jina lako kuu, na za mkono wako ulio hodari, na za mkono wako ulionyoshwa); atakapokuja na kuomba kuielekea nyumba hii; 43 basi, usikie huko mbinguni, makao yako, ukatende kwa kadiri ya yote atakayokuomba mgeni huyo; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe kama watu wako Israeli, nao wajue ya kuwa nyumba hii, niliyoijenga, imeitwa kwa jina lako. 44 Ikiwa watu wako watoka kwenda kupigana na adui zao, kwa njia yo yote utakayowapeleka, wakikuomba, Bwana, kuuelekea mji huu uliouchagua, na nyumba hii niliyoijenga kwa jina lako; 45 basi, uyasikie huko mbinguni maombi yao na dua yao, ukaitetee haki yao. 46 Ikiwa wamekutenda dhambi, (maana hakuna mtu asiyetenda dhambi), hata ukawaghadhibikia, ukawatia katika mikono ya adui zao, wawachukue mateka mpaka nchi ya adui zao, iliyo mbali au iliyo karibu; 47 basi, wakijirudia nafsi zao katika nchi ile watakayochukuliwa mateka, wakitubu, na kukusihi katika nchi ya hao waliowachukua mateka, wakisema, Tumekosa, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu; 48 watakaporejea kwako kwa mioyo yao yote, na kwa nia zao zote, katika nchi ya adui zao, waliowachukua mateka, wakikuomba, kwa kuikabili nchi yao, uliyowapa baba zao, na mji huu uliouchagua, na nyumba hii niliyoijenga kwa jina lako; 49 basi, uyasikie maombi yao na dua yao, huko mbinguni, makao yako, ukaitetee haki yao; 50 ukawasamehe watu wako waliokutenda dhambi, na makosa yao yote waliyokukosa; ukawape kuonewa huruma mbele yao waliowachukua mateka, ili wapate kuwahurumia. 51 Kwa kuwa ni watu wako, na urithi wako, uliowatoa katika Misri, toka katikati ya tanuu ya chuma. 52 Macho yako na yafumbuke, na kuielekea dua ya mtumwa wako, na dua za watu wako Israeli, ukawasikilize kila wakati watakapokulilia. 53 Kwa maana uliwatenga na watu wote wa dunia, wawe urithi wako, kama ulivyonena kwa mdomo wa Musa, mtumishi wako, hapo ulipowatoa baba zetu katika Misri, Ee Bwana MUNGU. 54 Hata ikawa, Sulemani alipokwisha kumwomba Bwana maombi hayo, na dua hiyo yote, akasimama na kuondoka hapo mbele ya madhabahu ya Bwana, hapo alipokuwa amepiga magoti, na kuikunjua mikono yake kuelekea mbinguni. 55 Akasimama, na kuwabariki mkutano wote wa Israeli kwa sauti kuu, akasema, 56 Na ahimidiwe Bwana, aliyewapa watu wake Israeli kustarehe, vile vile kama yote aliyoyaahidi. Halikukosa kupatikana neno lo lote katika ahadi yake njema, aliyoahidi kwa mkono wa Musa, mtumishi wake. 57 Bwana, Mungu wetu, na akae nasi, kama alivyokaa na baba zetu; asituache, wala asitutupe; 58 aielekeze mioyo yetu kwake, ili tuende katika njia zake zote, na kuzishika amri zake, na sheria zake, na hukumu zake, alizowaamuru baba zetu. 59 Na maneno yangu haya, niliyoyaomba mbele za Bwana, na yawe karibu na Bwana, Mungu wetu, mchana na usiku, ili aitetee haki ya mtumishi wake, na haki ya watu wake Israeli, kwa kadiri ya haja zao za kila siku. 60 Watu wote wa ulimwengu wajue ya kuwa Bwana ndiye Mungu; hakuna mwingine. 61 Mioyo yenu na iwe kamili kwa Bwana, Mungu wetu, kuenenda katika sheria zake, na kuzishika amri zake, kama ilivyo leo. 62 Ndipo mfalme, na Israeli wote pamoja naye, wakatoa sadaka mbele za Bwana. 63 Sulemani akatoa sadaka za amani, alizomtolea Bwana, ng'ombe ishirini na mbili elfu, na kondoo mia na ishirini elfu. Ndivyo mfalme na wana wa Israeli wote walivyoifanya wakfu nyumba ya Bwana. 64 Siku ile ile mfalme akaitakasa behewa ya katikati iliyokuwa mbele ya nyumba ya Bwana; kwa kuwa hapo ndipo alipotoa sadaka ya kuteketezwa, na sadaka ya unga, na mafuta ya sadaka za amani; kwa sababu ile madhabahu ya shaba iliyokuwa mbele za Bwana ilikuwa ndogo, haikutosha kuzipokea sadaka za kuteketezwa, na sadaka za unga, na mafuta ya sadaka za amani. 65 Basi, wakati ule Sulemani akafanya sikukuu, na Israeli wote pamoja naye, kusanyiko kubwa sana, kutoka maingilio ya Hamathi mpaka kijito cha Misri, mbele za Bwana, Mungu wetu, siku saba na siku saba, yaani siku kumi na nne. 66 Hata siku ya nane akaagana na watu, nao wakambarikia mfalme, wakaenda hemani kwao, wakifurahi na kuchangamka moyoni kwa wema wote Bwana aliomfanyia Daudi mtumishi wake, na Israeli watu wake. 66 On the eighth day he sent the people away: and they blessed the king, and went unto their tents joyful and glad of heart for all the goodness that the LORD had done for David his servant, and for Israel his people.

1 Wafalme 9

1 Ikawa Sulemani alipokwisha kuijenga nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme, na mambo yote yaliyoingia moyoni mwake Sulemani, naye akataka kuyafanya, 2 basi, Bwana akamtokea Sulemani mara ya pili kama alivyomtokea huko Gibeoni. 3 Bwana akamwambia, Nimeyasikia maombi yako na dua zako, ulizotoa mbele zangu. Nimeitakasa nyumba hii uliyoijenga ili niweke jina langu humo milele; tena macho yangu na moyo wangu utakuwapo hapo siku zote; 4 na wewe, ukienda mbele zangu kama alivyokwenda Daudi, baba yako, kwa ukamilifu wa moyo, na kwa adili, kufanya hayo yote niliyokuamuru, na kuzishika sheria zangu na hukumu zangu, 5 ndipo nitakapokifanya imara kiti cha ufalme wako juu ya Israeli milele; kama nilivyomwahidia Daudi, baba yako, nikisema, Hutakosa kuwa na mtu wa kukaa katika kiti cha enzi cha Israeli. 6 Bali mkighairi, mkaacha kunifuata, ninyi na watoto wenu, msizishike sheria zangu na amri zangu, nilizoziweka mbele yenu, tena mkienda na kuitumikia miungu mingine na kuiabudu, 7 basi nitawakatilia Israeli mbali na nchi hii niliyowapa; na nyumba hii niliyoitakasa kwa jina langu, nitaitupilia mbali na macho yangu, na Israeli watakuwa mithali na neno la tusi katika mataifa yote. 8 Na ijapokuwa nyumba hii imetukuka namna hii, lakini kila apitaye atasituka na kuizomea; nao watasema, Kwa nini Bwana ameitenda nchi hii na nyumba hii mambo haya? 9 Na watu watajibu, Kwa sababu walimwacha Bwana, Mungu wao, aliyewatoa baba zao katika nchi ya Misri, wakashikamana na miungu mingine na kuiabudu na kuitumikia, basi ndiyo sababu Bwana ameleta mabaya haya yote juu yao. 10 Ikawa miaka ishirini ilipopita, ambayo katika hiyo Sulemani alizijenga zile nyumba mbili, nyumba ya Bwana na nyumba yake mfalme, 11 (basi Hiramu, mfalme wa Tiro, alikuwa amemletea Sulemani mierezi na miberoshi, na dhahabu, sawasawa na haja zake zote), ndipo mfalme Sulemani akampa Hiramu miji ishirini ya nchi ya Galilaya. 12 Naye Hiramu akatoka Tiro kuitazama hiyo miji Sulemani aliyompa; wala haikumpendcza. 13 Akasema, Miji gani hii uliyonipa, ndugu yangu? Akaiita nchi ya Kabuli, hata leo. 14 Hiramu akamletea mfalme talanta sitini za dhahabu. 15 Na hii ndiyo sababu ya shokoa aliyoitoza mfalme Sulemani; ili kuijenga nyumba ya Bwana, na nyumba yake mwenyewe, na Milo, na ukuta wa Yerusalemu, na Hazori, na Megido, na Gezeri. 16 Farao, mfalme wa Misri, alikuwa amepanda akautwaa Gezeri, na kuuteketeza kwa moto, akawaua Wakanaani waliokaa mjini, akampa zawadi binti yake, mkewe Sulemani. 17 Naye Sulemani akaujenga Gezeri, na Beth-horoni wa chini, 18 na Baalathi, na Tamari ulio nyikani, katika nchi; 19 na miji yote ya hazina iliyokuwa yake Sulemani; na miji ya magari yake, na miji ya watu wake wapandao farasi, na kila alichopenda kujenga Sulemani huko Yerusalemu, na katika Lebanoni, na katika nchi yote ya mamlaka yake. 20 Kwa habari ya watu wote waliosalia, Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi, wasiokuwa wa wana wa Israeli; 21 watoto wao waliosalia baada yao katika nchi, ambao wana wa Israeli hawakuweza kuwaharibu kabisa, katika hao Sulemani akawatumikisha shokoa hata leo. 22 Lakini wa wana wa Israeli Sulemani hakumtumikisha mtu shokoa; ila ndio watu wa vita, na wangoje wake, na wakuu wake, na akida zake, na wakuu, wa magari yake, na wa wapanda farasi wake. 23 Hao maakida wakuu, waliokuwa juu ya kazi yake Sulemani, walikuwa mia tano na hamsini, waliowaamuru watu watendao kazi. 24 Lakini binti Farao akapanda toka mji wa Daudi, mpaka hiyo nyumba yake Sulemani, aliyomjengea; kisha, aliijenga Milo. 25 Na mara tatu kila mwaka Sulemani alikuwa akitoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani juu ya madhabahu aliyomjengea Bwana akafukiza uvumba pamoja nazo juu ya madhabahu iliyokuwako mbele za Bwana. Hivyo akaimaliza nyumba. 26 Tena, mfalme Sulemani akaunda merikebu huko Ezion-geberi, ulioko karibu na Elothi, pwani ya Bahari ya Shamu, katika nchi ya Edomu. 27 Naye Hiramu akatuma merikebuni watumishi wake, wanamaji wenye kuijua bahari, pamoja na watumishi wake Sulemani. 28 Wakafika Ofiri, wakachukua toka huko dhahabu, talanta mia nne na ishirini, wakamletea mfalme Sulemani.

1 Wafalme 10

1 Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo. 2 Akaingia Yerusalemu na wafuasi wengi sana, na ngamia wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia Sulemani, akazungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. 3 Naye Sulemani akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme asimwambie. 4 Naye malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani, na nyumba aliyokuwa ameijenga, 5 na chakula cha mezani pake, na watumishi wake walivyokaa, na kusimamia kwao wangoje wake, na mavazi yao, na wanyweshaji wake, na daraja yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana, roho yake ilizimia. 6 Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. 7 Lakini mimi sikuzisadiki habari hizo, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia. 8 Heri watu wako, na heri watumishi hawa wako, wasimamao mbele yako siku zote, wakisikia hekima yako. 9 Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli; kwa kuwa Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme, ufanye hukumu na haki. 10 Basi akampa mfalme talanta za dhahabu mia na ishirini, na manukato mengi, mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena wingi wa manukato, kama hayo malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani. 11 Tena merikebu za Hiramu, zilizochukua dhahabu kutoka Ofiri, zikaleta kutoka Ofiri miti ya msandali mingi sana, na vito vya thamani. 12 Mfalme akafanya kwa mia hiyo ya msandali nguzo za nyumba ya Bwana, na za nyumba ya mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala haikuja miti ya msandali kama hiyo, wala haikuonekana, hata leo. 13 Naye mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila alilotaka, zaidi ya hayo aliyopewa na Sulemani kwa ukarimu wake wa kifalme. Basi, akarudi akaenda zake katika nchi yake, yeye na watumishi wake. 14 Basi uzani wa dhahabu iliyomfikia Sulemani mwaka mmoja, ndio talanta mia sita sitini na sita, 15 zaidi ya faida ya wachuuzi, na bidhaa ya wafanya biashara, na ya wafalme wote wa hao waliochanganyika, na ya maliwali wa nchi. 16 Mfalme Sulemani akafanya ngao mia mbili za dhahabu iliyofuliwa; kila ngao moja ilipata shekeli mia sita za dhahabu. 17 Na vigao mia tatu vya dhahabu iliyofuliwa; kila kigao kimoja kilipata mane tatu za dhahabu. Mfalme akaviweka katika nyumba ya mwitu wa Lebanoni. 18 Tena mfalme akafanya kiti cha enzi kikubwa cha pembe, akakifunikiza kwa dhahabu iliyo safi. 19 Kiti kile kilikuwa na daraja sita, na juu yake kimeviringana nyuma; na mikono huko na huko mahali pa kuketi, na simba wawili wakisimama kando ya hiyo mikono. 20 Na simba kumi na wawili wamesimama juu ya daraja sita huko na huko; wala hakikufanyika kwa mkono wake katika ufalme wo wote. 21 Na vyombo vyote vya kunywea vya mfalme Sulemani vilikuwa vya dhahabu, na vyombo vyote vya nyumba ya mwitu wa Lebanoni vilikuwa vya dhahabu iliyosafika; hakuna vya fedha, fedha haikuhesabiwa kuwa kitu siku za Sulemani. 22 Kwa kuwa mfalme alikuwa na merikebu za Tarshishi baharini pamoja na merikebu za Hiramu; mara moja katika miaka mitatu huja merikebu za Tarshishi, zikileta dhahabu, na fedha, na pembe, na nyani, na tausi. 23 Basi mfalme Sulemani akawapita wafalme wote wa duniani kwa mali, na kwa hekima. 24 Ulimwengu wote ukamtafuta Sulemani uso wake, ili waisikie hekima yake, Mungu aliyomtia moyoni. 25 Wakaleta kila mtu zawadi yake, vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na mavazi, na silaha, na manukato, na farasi, na nyumbu, hesabu yake ya mwaka kwa mwaka. 26 Sulemani akakusanya magari na wapandao farasi; naye alikuwa na magari elfu na mia nne, na wapandao farasi kumi na mbili elfu, aliowaweka katika miji ya magari, na pamoja na mfalme huko Yerusalemu. 27 Mfalme akafanya fedha humo Yerusalemu kuwa kama mawe, na mierezi akaifinya kuwa kama mikuyu iliyomo Shefela, kwa kuwa mingi. 28 Nao farasi aliokuwa nao Sulemani wakaletwa toka Misri; wakapewa wafanya biashara wake mfalme kwa makundi, kila kundi na thamani yake. 29 Tena gari huja kutoka katika Misri kwa shekeli mia sita za fedha, na farasi mmoja kwa mia hamsini; vivyo watu wakawaletea wafalme wote wa Wahiti, na wafalme wa Shamu, mikononi mwao.

1 Wafalme 11

1 Mfalme Sulemani akawapenda wanawake wengi wageni, pamoja na binti yake Farao, wanawake wa Wamoabi, na wa Waamoni, na wa Waedomi, na wa Wasidoni, na wa Wahiti, 2 na wa mataifa Bwana aliyowaambia wana wa Israeli, Msiingie kwao, wala wasiingie kwenu; kwa kuwa hakika wataigeuza mioyo yenu kuifuata miungu yao. Sulemani akaambatana nao kwa kuwapenda. 3 Akawa na wake mia saba binti za kifalme, na masuria mia tatu; nao wakeze wakamgeuza moyo. 4 Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake. 5 Kwa kuwa Sulemani akamfuata Ashtorethi, mungu mke wa Wasidoni na Milkomu, chukizo la Waamoni. 6 Sulemani akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, wala hakumfuata Bwana kwa utimilifu, kama Daudi baba yake. 7 Sulemani akamjengea Kemoshi, chukizo la Wamoabi, mahali pa juu, katika mlima uliokabili Yerusalemu, na Moleki, chukizo la wana wa Amoni. 8 Na kadhalika ndivyo alivyowafanyia wake zake wa nchi za kigeni, waliofukiza uvumba, wakawatolea miungu yao dhabihu. 9 Basi Bwana akamghadhibikia Sulemani kwa sababu moyo wake umegeuka, naye amemwacha Bwana, Mungu wa Israeli, aliyemtokea mara mbili, 10 akamwamuru katika habari ya jambo lilo hilo asifuate miungu mingine; lakini yeye hakuyashika aliyoyaamuru Bwana. 11 Kwa hiyo Bwana akamwambia Sulemani, Kwa kuwa umefanya hayo, wala hukuyashika maagano yangu, na sheria zangu nilizokuamuru, hakika nitaurarua ufalme usiwe wako, nami nitampa mtumishi wako. 12 Walakini katika siku zako sitafanya haya, kwa ajili ya Daudi baba yako; nitaurarua utoke katika mkono wa mwana wako. 13 Lakini sitauondoa ufalme wote pia; nitampa mwana wako kabila moja, kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu, na kwa ajili ya Yerusalemu niliouchagua. 14 Ndipo Bwana akamwondokeshea Sulemani adui, Hadadi Mwedomi; yeye alikuwa wa wazao wake mfalme wa Edomu. 15 Kwa maana ikawa, Daudi alipokuwako Edomu, naye Yoabu, mkuu wa jeshi, amepanda awazike waliouawa, akiisha kumpiga kila mwanamume wa Edomu, 16 (kwa kuwa Yoabu alikaa huko miezi sita pamoja na Israeli wote, hata alipompoteza kila mwanamume wa Edomu); 17 yule Hadadi alikimbia, yeye na Waedomi wengine, watumishi wa baba yake, pamoja naye, waende Misri; yule Hadadi akali ni mtoto mdogo. 18 Wakaondoka katika Midiani, wakafika Parani; wakachukua pamoja nao watu toka Parani, wakafika Misri, kwa Farao mfalme wa Misri; aliyempa nyumba, akamwamria vyakula, akampa mashamba. 19 Hadadi akapendeza sana machoni pa Farao, hata akamwoza umbu la mkewe, umbu la Tapenesi aliyekuwa malkia. 20 Naye huyo umbu la Tapenesi akamzalia Genubathi mwanawe, ambaye Tapenesi alimlea nyumbani mwa Farao; naye Genubathi akawako nyumbani mwa Farao pamoja na wana wa Farao. 21 Naye Hadadi aliposikia huko Misri ya kuwa Daudi amelala na babaze, na Yoabu, jemadari wa jeshi, amekufa, Hadadi akamwambia Farao, Unipe ruhusa, niende mpaka nchi yangu. 22 Farao akamwambia, Umekosa nini kwangu, hata, tazama, unatafuta kuirudia nchi yako? Akajibu, Hakuna, lakini unipe ruhusa tu. 23 Tena, Mungu akamwondokeshea adui mwingine, Rezoni mwana wa Eliada, aliyemkimbia bwana wake Hadadezeri mfalme wa Soba, 24 naye akakusanya watu, akawa mkuu wa jeshi, hapo Daudi alipowaua hao watu wa Soba; wakaenda Dameski, wakakaa humo, na kumiliki huko Dameski. 25 Naye akawa adui wa Israeli siku zote za Sulemani, zaidi ya madhara yake Hadadi; naye akawachukia Israeli, akamiliki juu ya Shamu. 26 Na Yeroboamu wa Nebati, Mwefraimu wa Sereda, mtumwa wake Sulemani; ambaye jina lake mamaye aliitwa Serua, mwanamke aliyefiwa na mumewe; yeye naye akainua mkono wake juu ya mfalme. 27 Na hii ndiyo sababu ya yeye kumwinulia mfalme mkono. Sulemani aliijenga Milo, akapafunga palipobomoka pa mji wa baba yake Daudi. 28 Na huyo Yeroboamu alikuwa mtu hodari, shujaa; Sulemani akaona ya kuwa kijana huyo ni mtu mwenye bidii, akamweka juu ya kazi yote ya nyumba ya Yusufu. 29 Ikawa zamani zile Yeroboamu alipokuwa akitoka katika Yerusalemu, nabii Ahiya, Mshiloni, alikutana naye njiani; naye Ahiya amevaa vazi jipya, na hao wawili walikuwa peke yao mashambani. 30 Ahiya akalishika lile vazi jipya alilokuwa amelivaa, akalirarua vipande kumi na viwili. 31 Akamwambia Yeroboamu, Twaa wewe vipande kumi, maana Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nitaurarua ufalme, na kuuondoa katika mkono wa Sulemani, nami nitakupa wewe kabila kumi, 32 (lakini yeye atakuwa na kabila moja kwa ajili ya mtumishi wangu Daudi, na kwa ajili ya Yerusalemu mji ule niliouchagua katika miji yote ya kabila za Israeli); 33 kwa sababu wameniacha mimi wakaabudu Ashtorethi, mungu mke wa Wasidoni, na Kemoshi, mungu wa Wamoabi, na Milkomu, mungu wa wana wa Amoni wala hawakuenda katika njia zangu, kutenda mema machoni pangu, kuzishika sheria zangu na hukumu zangu, kama Daudi baba yake. 34 Walakini sitauondoa ufalme wote katika mkono wake; lakini nitamfanya awe mkuu siku zote za maisha yake, kwa ajili ya mtumishi wangu Daudi niliyemchagua kwa maana alizishika amri zangu na sheria zangu, 35 lakini nitauondoa ufalme katika mkono wa mwanawe, nami nitakupa wewe kabila kumi. 36 Nami nitampa mwana wake kabila moja, ili Daudi, mtumishi wangu, apate kuwa na taa siku zote mbele zangu katika Yerusalemu, mji ule niliouchagua niweke jina langu huko. 37 Nami nitakutwaa wewe, nawe utatawala kama roho yako inavyotamani, nawe utakuwa mfalme juu ya Israeli. 38 Tena itakuwa, ukiyasikia yote nitakayokuamuru, na kuenda katika njia zangu, na kutenda yaliyo mema machoni pangu, ili kuzishika amri zangu na hukumu zangu kama Daudi mtumishi wangu alivyotenda, basi, nitakuwa pamoja nawe, nitakujengea nyumba iliyo imara, kama nilivyomjengea Daudi, nami nitakupa wewe Israeli. 39 Tena nitawatesa wazao wa Daudi kwa sababu hii, lakini si daima. 40 Basi Sulemani akataka kumwua Yeroboamu, lakini Yeroboamu akaondoka, akakimbilia Misri, kwa Shishaki, mfalme wa Misri, akakaa katika Misri hata wakati wa kufa kwake Sulemani. 41 Nayo yaliyosalia ya Sulemani, mambo yake na yote aliyoyafanya, na hekima yake, je! Hayo siyo yaliyoandikwa kitabuni mwa mambo yake Sulemani? 42 Na siku alizotawala Sulemani katika Yerusalemu juu ya Israeli wote zilikuwa miaka arobaini. 43 Naye Sulemani akalala na baba zake, akazikwa katika mji wa Daudi baba yake; na Rehoboamu mwanawe akatawala mahali pake.

1 Wafalme 12

1 Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekwenda Shekemu, ili kumfanya mfalme. 2 Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari (maana alikuwa akaliko Misri, huko alikokimbilia awe mbali na mfalme Sulemani; Yeroboamu akakaa huko Misri, 3 wakapeleka watu kwenda kumwita); basi Yeroboamu na jamii yote ya Israeli wakaenda, wakamwambia Rehoboamu, wakasema, 4 Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia. 5 Akawaambia, Enendeni zenu hata siku ya tatu, kisha mnirudie tena. Watu wakaenda zao. 6 Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa? 7 Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima. 8 Lakini akaliacha shauri lile la wazee, walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, na kusimama mbele yake. 9 Akawaambia, Mwanipa shauri gani ili tuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakinena Utufanyie jepesi kongwa lile alilotutwika baba yako? 10 Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliokuambia, wakisema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, bali wewe utufanyie jepesi, uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. 11 Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. 12 Basi, Yeroboamu na watu wote wakamfikia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu. 13 Mfalme akawajibu watu wale kwa ukali, akaliacha shauri lile wazee walilompa; 14 akawajibu kama vile walivyomshauri vijana, akasema, Baba yangu alilifanya zito kongwa lenu, bali mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. 15 Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Bwana, ili alitimize neno lake, Bwana alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa kinywa cha Ahiya Mshiloni. 16 Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hakuwasikia, hao watu walimjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese. Haya! Nendeni zenu hemani kwenu, enyi Israeli; sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi. Hivyo Israeli wakaenda zao hemani kwao. 17 Lakini kwa habari za wana wa Israeli waliokaa katika miji ya Yuda, Rehoboamu aliwatawala wao. 18 Ndipo mfalme Rehoboamu akampeleka Adoramu, aliyekuwa juu ya shokoa, nao Israeli wote wakampiga kwa mawe hata akafa. Mfalme Rehoboamu akafanya haraka kupanda katika gari, ili akimbilie Yerusalemu. 19 Hivyo Israeli wakaasi juu ya nyumba ya Daudi hata leo. 20 Ikawa, Israeli wote waliposikia ya kwamba Yeroboamu amerudi, wakapeleka watu wakamwita aje mkutanoni, wakamfanya mfalme juu ya Israeli wote; wala hapakuwa na mtu aliyeshikamana na nyumba ya Daudi, ila kabila ya Yuda peke yake. 21 Hata Rehoboamu alipofika Yerusalemu, akakusanya nyumba yote ya Yuda, pamoja na kabila ya Benyamini, watu wateule mia na themanini elfu, waliokuwa watu wa vita, ili wapigane na nyumba ya Israeli, waurudishe ufalme tena kwa Rehoboamu mwana wa Sulemani. 22 Lakini likaja neno la Mungu kwa Shemaya mtu wa Mungu, kusema, 23 Mwambie Rehoboamu mwana wa Sulemani, mfalme wa Yuda, na jamaa yote ya Yuda na Benyamini, na watu waliosalia, ukisema, 24 Bwana asema hivi, Msiende, wala msipigane na ndugu zenu wana wa Israeli; rudini kila mtu nyumbani kwake; kwa kuwa jambo hili limetoka kwangu. Basi, wakalisikiliza neno la Bwana, wakarudi, wakaenda zao, sawasawa na neno la Bwana. 25 Ndipo Yeroboamu akajenga Shekemu katika milima ya Efraimu, akakaa huko. Akatoka huko akajenga Penueli. 26 Yeroboamu akasema moyoni mwake, Basi ufalme utairudia nyumba ya Daudi. 27 Kama watu hawa wakipanda kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Bwana huko Yerusalemu, ndipo mioyo ya watu hawa itamrudia bwana wao, yaani Rehoboamu, mfalme wa Yuda; nao wataniua mimi, na kumrudia Rehoboamu, mfalme wa Yuda. 28 Kwa hiyo mfalme akafanya shauri, akafanyiza ng'ombe wawili wa dhahabu, akawaambia watu, Ni vigumu kwenu kupanda kwenda Yerusalemu; tazama, hii ndiyo miungu yenu, enyi Israeli, iliyowapandisha kutoka nchi ya Misri. 29 Akamweka mmoja katika Betheli, na wa pili akamweka katika Dani. 30 Jambo hili likawa dhambi, maana watu walikwenda kuabudu mbele ya kila mmoja, hata huko Dani. 31 Tena akafanya nyumba za mahali pa juu, akafanya na watu wo wote, watu wasio wa wana wa Lawi, kuwa makuhani. 32 Yeroboamu akaamuru kushika sikukuu katika mwezi wa nane, siku ya kumi na tano ya mwezi, mfano wa sikukuu iliyokuwa katika Yuda, akapanda juu ili kuiendea madhabahu. Akafanya vivyo katika Betheli akiwatolea dhabihu wale ng'ombe aliowafanya; akawaweka katika Betheli wale makuhani wa mahali pa juu alipokuwa amepafanya. 33 Akatoa dhabihu juu ya ile madhabahu aliyoifanya katika Betheli, siku ya kumi na tano ya mwezi wa nane, mwezi aliouwaza moyoni mwake mwenyewe; akawaamuru wana wa Israeli waishike sikukuu hiyo, akapanda kuiendea madhabahu, ili kufukiza uvumba.

1 Wafalme 13

1 Na tazama, akatoka mtu wa Mungu katika Yuda kwa neno la Bwana, akafika Betheli. Naye Yeroboamu alikuwa akisimama penye madhabahu, afukize uvumba. 2 Basi mtu huyo akapiga kelele juu ya madhabahu, kwa neno la Bwana akasema, Ee madhabahu, madhabahu, Bwana asema hivi, Angalia, mtoto atazaliwa katika nyumba ya Daudi, jina lake Yosia; na juu yako atawachinja makuhani wa mahali pa juu, wanaofukiza uvumba juu yako, na mifupa ya watu itateketezwa juu yako. 3 Akatoa ishara siku ile ile, akasema, Hii ndiyo ishara aliyoinena Bwana, Tazama, madhabahu itapasuka, na majivu yaliyo juu yake yatamwagika. 4 Ikawa, mfalme Yeroboamu alipoyasikia maneno ya yule mtu wa Mungu, alipopiga kelele juu ya madhabahu huko Betheli, alinyosha mkono wake pale madhabahuni, akasema, Mkamateni. Basi ule mkono wake aliounyosha ukakatika, wala hakuweza kuurudisha kwake tena. 5 Madhabahu ikapasuka, majivu ya madhabahuni yakamwagika, sawasawa na ishara aliyoitoa mtu wa Mungu kwa neno la Bwana. 6 Mfalme akajibu, akamwambia yule mtu wa Mungu, Umsihi sasa Bwana, Mungu wako, ukaniombee, ili nirudishiwe mkono wangu tena. Yule mtu wa Mungu akamwomba Bwana mkono wa mfalme ukarudishwa tena, ukawa kama ulivyokuwa kwanza. 7 Mfalme akamwambia mtu wa Mungu, Karibu nyumbani kwangu ujiburudishe, nami nitakupa thawabu. 8 Mtu wa Mungu akamwambia mfalme, Ujaponipa nusu ya nyumba yako, sitaingia pamoja nawe, wala sitakula chakula, wala sitakunywa maji mahali hapa; 9 maana ndivyo nilivyoagizwa kwa neno la Bwana, kusema, Usile chakula cho chote wala usinywe maji, wala usirudi kwa njia ile uliyoijia. 10 Basi akaenda zake kwa njia nyingine, wala hakurudi kwa njia ile aliyoijia Betheli. 11 Basi nabii mmoja mzee alikuwa akikaa katika Betheli; na wanawe wakamwendea wakamwambia kila neno alilolitenda yule mtu wa Mungu siku ile katika Betheli; na maneno aliyomwambia mfalme, hayo nayo walimwambia baba yao. 12 Baba yao akawaambia, Amekwenda zake kwa njia ipi? Kwa maana wanawe walikuwa wameiona njia ile aliyoiendea yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda. 13 Akawaambia wanawe, Nitandikieni punda. Wakamtandikia punda, naye akampanda. 14 Akamfuata mtu wa Mungu, akamkuta ameketi chini ya mwaloni, akamwambia, Je! Wewe ndiwe yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda? Akamwambia, Mimi ndiye. 15 Akamwambia, Karibu kwangu nyumbani, ule chakula. 16 Naye akamwambia, Siwezi kurudi pamoja nawe, wala kuingia pamoja nawe; wala sili chakula wala sinywi maji pamoja nawe hapa; 17 kwani nimeambiwa kwa neno la Bwana, Usile chakula wala usinywe maji huko, wala usirudi kwa njia ile uliyoijia. 18 Akamwambia, Mimi nami ni nabii kama wewe, na malaika akaniambia kwa neno la Bwana, kusema, Mrudishe pamoja nawe nyumbani kwako, ale chakula, akanywe maji. Lakini alisema uongo. 19 Basi mtu yule akarudi pamoja naye, akala chakula, akanywa maji nyumbani mwake. 20 Hata ikawa, walipokuwa wameketi mezani, neno la Bwana likamjia nabii yule aliyemrudisha; 21 akamlilia yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda, akinena, Bwana asema hivi, Kwa sababu umeiasi kauli ya Bwana, wala hukuishika amri ile aliyokuamuru Bwana, Mungu wako, 22 bali umerudi, ukala chakula ukanywa maji, hapo alipokuambia, Usile chakula, wala usinywe maji; maiti yako haitaliingia kaburi la baba zako. 23 Basi ikawa, alipokwisha kula chakula na kunywa maji, yule nabii aliyemrudisha akamtandikia punda. 24 Na alipokuwa amekwenda zake, simba alimkuta njiani, akamwua. Maiti yake ikatupwa njiani, na yule punda akasimama karibu naye; na yule simba naye akasimama karibu na maiti. 25 Na tazama, watu wakapita, wakauona mzoga umetupwa njiani, na yule simba akisimama karibu na mzoga, wakaenda, wakatoa habari katika mji ule alimokaa yule nabii mzee. 26 Na yule nabii aliyemrudisha njiani alipopata habari, akasema; Ndiye yule mtu wa Mungu, aliyeiasi kauli ya Bwana; kwa hiyo Bwana amempambanisha na simba, simba akamrarua, akamwua, sawasawa na neno la Bwana alilomwambia. 27 Akawaambia wanawe, akasema, Nitandikieni punda. Wakamtandikia. 28 Akaenda, akamwona yule maiti ametupwa njiani, na punda na simba wamesimama karibu na maiti; yule simba alikuwa hakumla maiti, wala hakumrarua punda. 29 Nabii yule akamtwaa maiti wa yule mtu wa Mungu, akamweka juu ya punda wake, akamrudisha; yule nabii mzee akaenda mjini mwake, kukaa matanga, na kumzika. 30 Akamweka maiti katika kaburi lake mwenyewe; wakamlilia, wakisema, Aa! Ndugu yangu! 31 Hata ikawa, alipokwisha kumzika, akawaambia wanawe, akasema, Nikifa mimi, nizikeni katika kaburi hili alimozikwa yule mtu wa Mungu; iwekeni mifupa yangu kando ya mifupa yake. 32 Kwa maana neno hilo alilolia juu ya madhabahu katika Betheli, kwa neno la Bwana, na juu ya nyumba zote za mahali pa juu zilizo katika miji ya Samaria, hakika litatimizwa. 33 Baada ya hayo Yeroboamu hakuiacha njia yake mbovu, lakini akafanya tena makuhani wa mahali pa juu, wa watu wo wote. 34 Kila aliyetaka akamfanya wakfu, ili wawepo makuhani wa mahali pa juu. Jambo hilo likawa dhambi kwa nyumba ya Yeroboamu, hata kuiharibu, na kuifuta usoni pa nchi.

1 Wafalme 14

1 Siku zile akaugua Abiya, mwana wa Yeroboamu. 2 Yeroboamu akamwambia mkewe, Ondoka, tafadhali, ujibadilishe, wasikujue kuwa mkewe Yeroboamu; ukaende Shilo; tazama, yuko huko Ahiya nabii, aliyeninena mimi ya kwamba nitakuwa mfalme juu ya watu hawa. 3 Twaa mkononi mikate kumi, na kaki, na mtungi wa asali, ukamwendee; naye atakuambia kijana atakuwaje. 4 Akafanya hivi mkewe Yeroboamu, akaondoka, akaenda Shilo, akaja nyumbani kwa Ahiya. Basi Ahiya hakuweza kuona; kwa kuwa macho yake yamepofuka kwa sababu ya uzee wake. 5 Bwana akamwambia Ahiya, Angalia, mkewe Yeroboamu anakuja akuulize mambo ya mwanawe; kwa maana hawezi; hivi na hivi umwambie; kwani itakuwa akiingia atajifanya kuwa mwanamke mwingine. 6 Ikawa, Ahiya alipoisikia sauti ya miguu yake, akiingia mlangoni, alisema, Karibu, mkewe Yeroboamu; mbona wajifanya kuwa mwingine maana nimetumwa kwako wewe, mwenye maneno mazito. 7 Nenda, umwambie Yeroboamu, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa kuwa nilikutukuza miongoni mwa watu, nikakufanya uwe mkuu juu ya watu wangu Israeli, 8 nikaurarulia mbali ufalme utoke nyumba yake Daudi, na kukupa wewe; walakini wewe hukuwa kama mtumishi wangu Daudi, aliyezishika amri zangu, na kunifuata kwa moyo wake wote, asifanye lo lote ila yaliyo mema machoni pangu; 9 lakini umekosa kuliko wote waliokutangulia, umekwenda kujifanyia miungu mingine, na sanamu zilizoyeyuka, unikasirishe, na kunitupa nyuma yako; 10 tazama, kwa hiyo mimi nitaleta mabaya juu ya nyumba yake Yeroboamu, nami nitamkatia Yeroboamu kila mwanamume, aliyefungwa na aliyeachwa katika Israeli, nami kuondoa nitawaondoa waliobaki wa nyumba yake Yeroboamu, kama mtu aondoavyo mavi, hata itakapokwisha pia. 11 Yeye afaye wa Yeroboamu mjini mbwa watamla; afaye mashambani ndege wa angani watamla; kwa kuwa Bwana amelinena hilo. 12 Basi ondoka, urudi nyumbani kwako; na miguu yako itakapoingia mjini huyo kijana atakufa. 13 Na Israeli wote watamlilia, na kumzika, kwa maana ndiye peke yake wa Yeroboamu atakayeingia kaburini; kwa sababu limeonekana ndani yake jambo lililo jema kwa Bwana, Mungu wa Israeli, nyumbani mwa Yeroboamu. 14 Tena Bwana atajiinulia mfalme wa Israeli atakayeiharibu nyumba ya Yeroboamu siku ile; na nini tena hata sasa? 15 Kwa kuwa Bwana atawapiga Israeli kama manyasi yatikiswavyo majini; naye atawang'oa Israeli katika nchi hii njema, aliyowapa baba zao, naye atawatawanya ng'ambo ya Mto; kwa sababu wamejifanyia maashera yao, wakimkasirisha Bwana. 16 Naye atawatoa Israeli kwa ajili ya makosa ya Yeroboamu, aliyoyakosa, ambayo kwa hayo amewakosesha Israeli. 17 Basi mkewe Yeroboamu akaondoka, akaenda zake, akafika Tirza; naye alipofika kizingitini kwa nyumba, huyo kijana akafa. 18 Israeli wote wakamzika, wakamlilia; sawasawa na neno la Bwana, alilolinena kwa mkono wa mtumishi wake Ahiya nabii. 19 Na mambo yake Yeroboamu yaliyosalia, ya kupigana na ya kutawala, tazama, yameandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli. 20 Na siku alizotawala Yeroboamu zilikuwa miaka ishirini na miwili; akalala na babaze, naye Nadabu mwanawe akatawala mahali pake. 21 Naye Rehoboamu mwana wa Sulemani akatawala katika Yuda. Rehoboamu akaanza kutawala alipokuwa mwenye miaka arobaini na mmoja, akatawala miaka kumi na saba huko Yerusalemu, mji aliouchagua Bwana miongoni mwa kabila zote za Israeli, ili aliweke jina lake huko. Na jina la mamaye aliitwa Naama, Mwamoni. 22 Basi Yuda wakafanya maovu machoni pa Bwana; wakamtia wivu, kwa makosa yao waliyoyakosa, kuliko yote waliyoyafanya baba zao. 23 Maana hao pia wakajijengea mahali pa juu, na nguzo, na maashera, juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi. 24 Na mahanithi walikuwako katika nchi, wakafanya sawasawa na machukizo yote ya mataifa Bwana aliowafukuza mbele ya wana wa Israeli. 25 Ikawa, mwaka wa tano wa mfalme Rehoboamu, akapanda Shishaki, mfalme wa Misri, juu ya Yerusalemu; 26 akazichukua hazina za nyumba ya Bwana, na hazina za nyumba ya mfalme; akazichukua zote. Akazichukua pia ngao zote za dhahabu alizozifanya Sulemani. 27 Mfalme Rehoboamu akafanya ngao za shaba mahali pake, akawakabidhi wakuu wa walinzi, waliongoja mlangoni pa nyumba ya mfalme. 28 Ikawa kila wakati mfalme alipoingia nyumbani mwa Bwana, hao walinzi walizichukua; wakazirudisha tena katika chumba cha walinzi. 29 Na mambo yake Rehoboamu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 30 Kulikuwa na vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu siku zote. 31 Rehoboamu akalala na babaze, akazikwa pamoja na babaze mjini mwa Daudi. Na jina la mamaye aliitwa Naama, Mwamoni. Na mwanawe, Abiya, alitawala mahali pake.

1 Wafalme 15

1 Mwaka wa kumi na nane wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, Abiya alianza kutawala juu ya Yuda. 2 Miaka mitatu akatawala huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Maaka, binti Absalomu. 3 Akaziendea dhambi zote za babaye, alizozifanya kabla yake; wala moyo wake haukuwa mkamilifu na Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi babaye. 4 Walakini kwa ajili ya Daudi, Bwana, Mungu wake, akampa taa humo Yerusalemu, amwinue mwanawe baada yake, na kuufanya imara Yerusalemu; 5 kwa sababu Daudi alifanya yaliyo mema machoni pa Bwana, wala hakukosa katika yote aliyomwamuru, siku zote za maisha yake, isipokuwa katika habari ya Uria, Mhiti. 6 Basi kulikuwa na vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu siku zote za maisha yake. 7 Na mambo yote ya Abiya yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? Kulikuwa na vita kati ya Abiya na Yeroboamu. 8 Abiya akalala na baba zake, wakamzika mjini mwa Daudi. Akatawala Asa mwanawe mahali pake. 9 Mwaka wa ishirini wa Yeroboamu mfalme wa Israeli, Asa alianza kutawala juu ya Yuda. 10 Akatawala miaka arobaini na mmoja huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Maaka, binti Absalomu. 11 Basi, Asa akafanya yaliyo mema machoni pa Mungu, kama alivyofanya babaye Daudi. 12 Akawafukuza mahanithi katika nchi, akaziondoa sanamu zote walizozifanya baba zake. 13 Hata na Maaka, mamaye, akamwondolea daraja yake asiwe malkia, kwa kuwa amefanya sanamu ya kuchukiza kwa Ashera; basi Asa akaikata sanamu yake akaiteketeza penye kijito cha Kidroni. 14 Lakini mahali pa juu hapakuondoshwa; ila moyo wake Asa ulikuwa mkamilifu kwa Bwana siku zake zote. 15 Akavileta vile vitu alivyovitakasa baba yake, na vile alivyovitakasa yeye mwenyewe, katika nyumba ya Bwana, fedha; na dhahabu, na vyombo. 16 Kulikuwa na vita kati ya Asa na Baasha mfalme wa Israeli siku zao zote. 17 Kisha, Baasha mfalme wa Israeli akaondoka juu ya Yuda, akaujenga Rama, ili asimwache mtu ye yote kutoka wala kuingia kwa Asa mfalme wa Yuda. 18 Ndipo Asa akazitwaa fedha zote na dhahabu zilizosalia katika hazina za nyumba ya Bwana, na hazina za nyumba ya mfalme, akazitia mikononi mwa watumishi wake; mfalme Asa akawatuma kwa Ben-hadadi, mwana wa Tabrimoni, mwana wa Hezioni, mfalme wa Shamu, aliyekaa Dameski, akasema, 19 Tumepatana mimi nawe, na baba yangu na baba yako; angalia, nimekuletea zawadi, fedha na dhahabu; basi nenda, uyavunje mapatano yako na Baasha mfalme wa Israeli, ili aniondokee mimi. 20 Naye Ben-hadadi akamsikiliza mfalme Asa, akawatuma wakuu wa majeshi yake juu ya miji ya Israeli, akapiga Iyoni, na Dani, na Abel-beth-maaka na Kinerothi yote, na nchi yote ya Naftali. 21 Ikawa Baasha aliposikia habari hiyo akaacha kuujenga Rama, akaenda akakaa Tirza. 22 Ndipo mfalme Asa akatangaza kwa Yuda pia; asiachiliwe mtu; nao wakayachukua mawe ya Rama na miti yake, aliyoijengea Baasha; naye mfalme Asa akajenga kwa vitu hivyo Geba wa Benyamini na Mispa. 23 Na mambo yote ya Asa yaliyosalia, na nguvu zake zote, na yote aliyoyafanya, na miji aliyoijenga, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? Lakini alipokuwa mzee alikuwa na ugonjwa wa miguu. 24 Asa akalala na babaze, akazikwa pamoja na babaze mjini mwa Daudi baba yake. Na Yehoshafati mwanawe akatawala mahali pake. 25 Nadabu mwana wa Yeroboamu alianza kutawala juu ya Israeli, mwaka wa pili wa Asa mfalme wa Yuda, akatawala juu ya Israeli miaka miwili. 26 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, akaiendea njia ya baba yake, na kosa lake alilowakosesha Israeli. 27 Basi Baasha wa Ahiya, wa mbari ya Isakari, akamfanyia fitina; Baasha akampiga huko Gibethoni ulio wa Wafilisti; kwani Nadabu na Israeli wote walikuwa wakiuhusuru Gibethoni. 28 Mwaka wa tatu wa Asa mfalme wa Yuda Baasha akamwua, akatawala mahali pake. 29 Ikawa mara alipotawala, akawapiga nyumba yote ya Yeroboamu. Hakumwachia Yeroboamu mwenye pumzi ye yote, hata alipomharibu sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa mtumishi wake Ahiya, Mshiloni; 30 kwa sababu ya makosa yake Yeroboamu aliyoyakosa, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli; kwa sababu ya chukizo lake alilomchukiza Bwana, Mungu wa Israeli, hata kumghadhibisha. 31 Basi mambo yote ya Nadabu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 32 Kulikuwa na vita kati ya Asa na Baasha mfalme wa Israeli siku zao zote. 33 Katika mwaka wa tatu wa Asa mfalme wa Yuda, Baasha mwana wa Ahiya alianza kutawala juu ya Israeli wote huko Tirza, akatawala miaka ishirini na minne. 34 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana akaiendea njia ya Yeroboamu, na kosa lake ambalo kwa hilo aliwakosesha Israeli.

1 Wafalme 16

1 Ndipo neno la Bwana likamjia Yehu mwana wa Hanani juu ya Baasha, kusema, 2 Kwa kuwa mimi nilikuinua kutoka katika mavumbi, na kukufanya uwe mkuu juu ya watu wangu Israeli; nawe umeiendea njia ya Yeroboamu, na kuwakosesha watu wangu Israeli, hata wanighadhibishe kwa makosa yao; 3 angalia, kuondoa nitawaondoa Baasha na jamaa yake; tena nitaifanya nyumba yako iwe kama nyumba ya Yeroboamu mwana wa Nebati. 4 Mtu amfiaye Baasha mjini mbwa watamla; naye amfiaye mashambani ndege wa angani watamla. 5 Basi, mambo yote ya Baasha yaliyosalia, na aliyoyafanya, na nguvu zake, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 6 Baasha akalala na babaze, akazikwa katika Tirza; naye Ela mwanawe akatawala mahali pake. 7 Tena neno la Bwana likaja kwa mkono wa nabii Yehu mwana wa Hanani juu ya Baasha, na juu ya nyumba yake, kwa sababu ya mabaya yote aliyoyatenda machoni pa Bwana, akimghadhibisha kwa kazi ya mikono yake, kwa kufanana na nyumba ya Yeroboamu, na kwa sababu aliiharibu. 8 Katika mwaka wa ishirini na sita wa Asa mfalme wa Yuda, Ela mwana wa Baasha alianza kutawala juu ya Israeli huko Tirza, akatawala miaka miwili. 9 Na mtumwa wake Zimri, jemadari wa nusu ya magari yake, akamfanyia fitina; alipokuwako Tirza akinywa hata kulewa nyumbani mwa Arsa, aliyekuwa juu ya nyumba huko Tirza; 10 Zimri akaingia akampiga, akamwua, katika mwaka wa ishirini na saba wa Asa mfalme wa Yuda, akatawala mahali pake. 11 Ikawa, alipoanza kutawala, mara alipoketi juu ya kiti chake cha enzi, akawaua nyumba yote ya Baasha; hakumwachia mwanamume ye yote, wa jamaa zake, wala wa rafiki zake. 12 Hivyo Zimri akaiharibu nyumba yote ya Baasha, sawasawa na neno la Bwana, alilolinena juu ya Baasha kwa Yehu nabii, 13 kwa sababu ya makosa yake Baasha, na makosa yote ya Ela mwanawe, waliyoyakosa, na kuwakosesha Israeli, wakimghadhibisha Bwana, Mungu wa Israeli, kwa matendo yao ya ubatili. 14 Na mambo yote ya Ela yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 15 Katika mwaka wa ishirini na saba wa Asa mfalme wa Yuda, Zimri akatawala muda wa siku saba huko Tirza. Basi, watu walikuwa wametua maragoni kupigana na Gibethoni, ulio wa Wafilisti. 16 Na hao watu waliokuwako maragoni wakasikia habari ya kwamba Zimri amefanya fitina, tena amempiga mfalme; kwa hiyo Israeli wote wakamfanya Omri, jemadari wa jeshi, awe mfalme juu ya Israeli siku ile maragoni. 17 Omri akapanda kutoka Gibethoni, na Israeli wote pamoja naye, wakauhusuru Tirza. 18 Ikawa Zimri alipoona ya kuwa mji umetwaliwa, akaingia ngomeni mwa nyumba ya mfalme, akaiteketeza nyumba ya mfalme juu yake kwa moto, akafa; 19 kwa sababu ya makosa aliyoyakosa, akifanya mabaya machoni pa Bwana, kwa kuiendea njia ya Yeroboamu na makosa yake aliyoyafanya akiwakosesha Israeli. 20 Na mambo yote ya Zimri yaliyosalia na fitina yake aliyoifanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 21 Ndipo watu wa Israeli wakatengwa sehemu mbili; nusu ya watu wakamfuata Tibni mwana wa Ginathi, ili wamfanye mfalme; nusu wakamfuata Omri. 22 Lakini hao watu waliomfuata Omri wakawashinda watu waliomfuata Tibni mwana wa Ginathi; basi akafa Tibni, akatawala Omri. 23 Katika mwaka wa thelathini na moja wa Asa, mfalme wa Yuda, Omri alianza kutawala juu ya Israeli, akatawala miaka kumi na miwili. Akatawala huko Tirza miaka sita. 24 Kisha akanunua kilima cha Samaria kwa Shemeri kwa talanta mbili za fedha; akajenga juu ya kilima kile, akauita mji alioujenga Samaria, kwa kuliandama jina lake Shemeri, aliyekuwa mwenye kilima. 25 Omri akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, akatenda maovu kuliko wote waliomtangulia; 26 kwa kuwa aliiendea njia yote ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na makosa yake, aliyowakosesha Israeli, ili kumghadhibisha Bwana, Mungu wa Israeli, kwa matendo yao ya ubatili. 27 Nayo mambo yote ya Omri yaliyosalia aliyoyatenda, na uthabiti alioufanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 28 Omri akalala na babaze, akazikwa huko Samaria; na Ahabu mwanawe akatawala mahali pake. 29 Ahabu mwana wa Omri alianza kutawala juu ya Israeli katika mwaka wa thelathini na nane wa Asa mfalme wa Yuda; akatawala Ahabu mwana wa Omri juu ya Israeli katika Samaria miaka ishirini na miwili. 30 Ahabu mwana wa Omri akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana kuliko wote waliomtangulia. 31 Ikawa, kama ingalikuwa neno dogo tu kuyaendea makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, akamwoa Yezebeli binti Ethbaali, mfalme wa Wasidoni, akaenda akamtumikia Baali, akamsujudia. 32 Akamjengea Baali madhabahu katika nyumba ya Baali, aliyoijenga huko Samaria. 33 Ahabu akaifanya Ashera; Ahabu akazidi kumghadhibisha Bwana, Mungu wa Israeli, kuliko wafalme wote wa Israeli waliomtangulia. 34 Katika siku zake, Hieli Mbetheli akajenga Yeriko; akatia misingi yake kwa kufiwa na Abiramu mzaliwa wake wa kwanza, na kuyaweka malango yake kwa kufiwa na mwana wake mdogo Segubu; sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa Yoshua mwana wa Nuni.

1 Wafalme 17

1 Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu, Kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu. 2 Neno la Bwana likamjia, kusema, 3 Ondoka hapa, geuka, uende upande wa mashariki, ujifiche karibu na kijito cha Kerithi kinachokabili Yordani. 4 Itakuwa utakunywa maji ya kile kijito; nami nimewaamuru kunguru wakulishe huko. 5 Basi akaenda akafanya kama alivyosema Bwana; kwa kuwa akaenda akakaa karibu na kijito cha Kerithi, kinachokabili Yordani. 6 Kunguru wakamletea mkate na nyama asubuhi, na mkate na nyama jioni, akanywa maji ya kile kijito. 7 Ikawa, baada ya siku kupita, kile kijito kikakatika, kwa sababu mvua haikunyesha katika nchi. 8 Neno la Bwana likamjia, kusema, 9 Ondoka, uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko akulishe. 10 Basi, akaondoka, akaenda Sarepta; hata alipofika langoni pa mji, kumbe! Mwanamke mjane alikuwako akiokota kuni; akamwita, akamwambia, Niletee, nakuomba, maji kidogo chomboni nipate kunywa. 11 Alipokuwa akienda kuleta, akamwita akasema, Niletee, nakuomba, kipande cha mkate mkononi mwako. 12 Naye akasema, Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, sina mkate, ila konzi ya unga katika pipa, na mafuta kidogo katika chupa; nami ninaokota kuni mbili ili niingie nijipikie nafsi yangu na mwanangu, tuule tukafe. 13 Eliya akamwambia, Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao. 14 Kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi. 15 Basi akaenda, akafanya kama alivyosema Eliya; na yeye mwenyewe, na Eliya, na nyumba yake, wakala siku nyingi. 16 Lile pipa la unga halikupunguka, wala ile chupa ya mafuta haikuisha, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa kinywa cha Eliya. 17 Ikawa, baada ya hayo, mwana wake yule mwanamke, bibi wa nyumba ile, akaugua; ugonjwa wake ukazidi hata akawa hana pumzi tena. 18 Akamwambia Eliya, Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu? Je! Umenijia ili dhambi yangu ikumbukwe, ukamwue mwanangu? 19 Akamwambia, Nipe mwanao. Akamtoa katika kifua chake, akamchukua juu chumbani mle alimokaa mwenyewe, akamlaza kitandani pake. 20 Akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, je! Umemtenda mabaya mjane huyu ninayekaa kwake hata kumfisha mwanawe. 21 Akajinyosha juu ya mtoto mara tatu, akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, nakusihi, roho ya mtoto huyu imrudie ndani yake tena. 22 Bwana akaisikia sauti ya Eliya; na roho ya mtoto ikamrudia, akafufuka. 23 Eliya akamtwaa mtoto, akamchukua toka orofani mpaka chini ya nyumba ile, akampa mama yake. Eliya akanena, Tazama, mwanao yu hai. 24 Mwanamke akamwambia Eliya, Sasa najua ya kuwa wewe ndiwe mtu wa Mungu, na ya kuwa neno la Bwana kinywani mwako ni kweli.

1 Wafalme 18

1 Ikawa baada ya siku nyingi, neno la Bwana likamjia Eliya, katika mwaka wa tatu, kusema, Enenda, ukajionyeshe kwa Ahabu; nami nitaleta mvua juu ya nchi. 2 Basi Eliya akaenda ili ajionyeshe kwa Ahabu. Na njaa ilikuwa nzito katika Samaria. 3 Ahabu akamwita Obadia, aliyekuwa juu ya nyumba yake; (na huyu Obadia alikuwa mwenye kumcha Bwana sana; 4 kwa kuwa ikawa, Yezebeli alipowaua manabii wa Bwana, Obadia akatwaa manabii mia, akawaficha hamsini hamsini katika pango, akawalisha chakula na kuwapa maji). 5 Ahabu akamwambia Obadia, Pita katika nchi, kwenye chemchemi zote za maji, na vijito vyote; labda tutapata majani, tuwahifadhi hai farasi na nyumbu, tusipate hasara ya hao wanyama wote. 6 Basi wakaigawanya nchi, ili wapite katika nchi yote; Ahabu akaenda zake njia moja peke yake, na Obadia akaenda zake njia nyingine peke yake. 7 Na Obadia alipokuwa njiani, kumbe! Eliya akakutana naye. Akamtambua, akaanguka kifudifudi, akanena, Je! Ni wewe, bwana wangu Eliya? 8 Akamjibu, Ni mimi. Enenda, umwambie bwana wako, Tazama, Eliya yupo. 9 Akamwambia, Nimekosa nini, hata unitie mimi mtumishi wako mkononi mwa Ahabu, aniue? 10 Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, hakuna taifa wala ufalme ambao bwana wangu hakutuma watu wakutafute; na waliposema, Hayupo, akawaapisha ule ufalme, na taifa, ya kwamba hawakukuona. 11 Nawe sasa wasema, Enenda, umwambie bwana wako, Tazama, Eliya yupo. 12 Na itakuwa, mara mimi nikiondoka kwako, roho ya Bwana atakuchukua uende nisikojua; nami nitakapokwenda kumwambia Ahabu, naye asipokuona, ataniua, lakini mimi mtumishi wako namcha Bwana tangu ujana wangu. 13 Je! Bwana wangu hakuambiwa nilivyofanya hapo Yezebeli alipowaua manabii wa Bwana? Jinsi nilivyowaficha manabii wa Bwana, watu mia, hamsini hamsini katika pango, nikawalisha chakula na kuwapa maji? 14 Nawe sasa wasema, Enenda umwambie bwana wako, Tazama, Eliya yupo; basi, ataniua. 15 Eliya akasema, Kama Bwana wa majeshi aishivyo ambaye ninasimama mbele zake, hakika nitajionyesha kwake leo. 16 Basi, Obadia akaenda zake amwone Ahabu, akamwambia; naye Ahabu akaenda kumlaki Eliya. 17 Ikawa, Ahabu alipomwona Eliya, Ahabu akamwambia, Je! Ni wewe, Ewe mtaabishaji wa Israeli? 18 Naye akajibu, Si mimi niliyewataabisha Israeli; bali ni wewe, na nyumba ya baba yako, kwa kuwa mmeziacha amri za Bwana; nawe umewafuata mabaali. 19 Basi sasa upeleke watu, unikusanyie jamii ya Israeli katika mlima wa Karmeli, na wale manabii wa Baali mia nne na hamsini, na wale manabii wa Ashera mia nne, walao chakula mezani pa Yezebeli. 20 Basi, Ahabu akapeleka watu kwa wana wa Israeli wote, akawakusanya manabii pamoja katika mlima wa Karmeli. 21 Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. 22 Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. 23 Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. 24 Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri. 25 Eliya akawaambia manabii wa Baali, Jichagulieni ng'ombe mmoja, mkamtengeze kwanza; maana ninyi ndio wengi; mkaliitie jina la mungu wenu, wala msitie moto chini. 26 Wakamtwaa yule ng'ombe waliyepewa, wakamtengeza, wakaliitia jina la Baali tangu asubuhi hata adhuhuri, wakisema, Ee Baali, utusikie. Lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu. Nao wakaruka-ruka juu ya madhabahu waliyoifanya. 27 Ikawa, wakati wa adhuhuri, Eliya akawafanyia dhihaka, akasema, Mwiteni kwa sauti kuu; maana ni mungu huyo; labda anazungumza, au ana shughuli, au anasafiri, au labda amelala, sharti aamshwe. 28 Wakapiga kelele, wakajikata-kata kwa visu na vyembe kama ilivyo desturi yao, hata damu ikawachuruzika. 29 Ikawa, wakati wa adhuhuri ulipopita, walitabiri hata wakati wa kutoa dhabihu ya jioni; lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu, wala aliyeangalia. 30 Kisha Eliya akawaambia watu wote, Nikaribieni mimi. Watu wote wakamkaribia. Akaitengeneza madhabahu ya Bwana iliyovunjika. 31 Eliya akatwaa mawe kumi na mawili, kwa hesabu ya kabila za wana wa Yakobo, aliyejiliwa na neno la Bwana na kuambiwa, Jina lako litakuwa Israeli. 32 Naye akaijenga madhabahu kwa mawe hayo katika jina la Bwana; akafanya mfereji, kama wa vipimo viwili vya mbegu, ukiizunguka madhabahu. 33 Kisha akazipanga zile kuni, akamkata yule ng'ombe vipande vipande, akaviweka juu ya kuni. Akasema, Jazeni mapipa manne maji, mkayamwage juu ya sadaka ya kuteketezwa, na juu ya kuni. 34 Akasema, Fanyeni mara ya pili. Wakafanya mara ya pili. Akasema, Fanyeni mara ya tatu. Wakafanya mara ya tatu. 35 Yale maji yakaizunguka madhabahu; akaujaza mfereji maji. 36 Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli, na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. 37 Unisikie, Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, Bwana, ndiwe Mungu, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie. 38 Ndipo moto wa Bwana ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji. 39 Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu. 40 Eliya akawaambia, Wakamateni hao manabii wa Baali, asiokoke hata mmoja. Wakawakamata; na Eliya akawachukua mpaka kijito cha Kishoni, akawaua huko. 41 Naye Eliya akamwambia Ahabu, Haya! Inuka, ule, unywe; kwani pana sauti ya mvua tele. 42 Basi Ahabu akainuka ili ale na kunywa. Naye Eliya akapanda juu mpaka kilele cha Karmeli; akasujudu kifudifudi, akainama uso mpaka magotini. 43 Akamwambia mtumishi wake, Kwea sasa, utazame upande wa bahari. Akakwea, akatazama, na kusema, Hakuna kitu. Naye akanena, Enenda tena mara saba. 44 Ikawa mara ya saba akasema, Tazama, wingu linatoka katika bahari, nalo ni dogo kama mkono wa mtu. Akanena, Enenda, umwambie Ahabu, Tandika, ushuke, mvua isikuzuie. 45 Ikawa, muda si muda, mbingu zikawa nyeusi kwa mawingu na upepo, ikanyesha mvua nyingi. Ahabu akapanda garini, akaenda zake Yezreeli. 46 Mkono wa Bwana ulikuwa juu ya Eliya; akajikaza viuno, akapiga mbio mbele ya Ahabu mpaka kuiingia Yezreeli.

1 Wafalme 19

1 Basi, Ahabu akamwambia Yezebeli habari ya mambo yote aliyoyafanya Eliya, na jinsi alivyowaua manabii wote kwa upanga. 2 Ndipo Yezebeli akampelekea Eliya mjumbe, kusema, Miungu wanifanyie hivyo na kuzidi, nisipokufanya roho yako kesho, panapo wakati huu, kama roho ya mmojawapo wa hao. 3 Naye alipoona hayo, aliondoka, akaenda aihifadhi roho yake, akafika Beer-sheba, mji wa Yuda, akamwacha mtumishi wake huko. 4 Lakini yeye mwenyewe akaendelea katika jangwa mwendo wa siku moja, akaenda akaketi chini ya mretemu. Akajiombea roho yake afe, akasema, Yatosha; sasa, Ee Bwana, uiondoe roho yangu; kwa kuwa mimi si mwema kuliko baba zangu. 5 Naye akajinyosha akalala chini ya mretemu; na tazama, malaika akamgusa, akamwambia, Inuka, ule. 6 Akatazama, kumbe! Pana mkate umeokwa juu ya makaa, na gudulia la maji, kichwani pake. Akala, akanywa, akajinyosha tena. 7 Malaika wa Bwana akamwendea mara ya pili, akamgusa, akasema, Inuka, ule; maana safari hii ni kubwa mno kwako. 8 Akainuka, akala, akanywa, akaenda katika nguvu za chakula hicho siku arobaini mchana na usiku hata akafika Horebu, mlima wa Mungu. 9 Akafika kunako pango, akalala ndani yake. Na tazama, neno la Bwana likamjia, naye akamwambia, Unafanya nini hapa, Eliya? 10 Akasema, Nimeona wivu mwingi kwa ajili ya Bwana Mungu wa majeshi; kwa kuwa wana wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu; nao wanitafuta roho yangu, waiondoe. 11 Akasema, Toka, usimame mlimani mbele za Bwana. Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunja-vunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule; na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi; 12 na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu. 13 Ikawa, Eliya alipoisikia, alijifunika uso wake katika mavazi yake, akatoka, akasimama mlangoni mwa pango. Na tazama, sauti ikamjia, kusema, Unafanya nini hapa, Eliya? 14 Akasema, Nimeona wivu mwingi kwa ajili ya Bwana, Mungu wa majeshi; kwa kuwa wana wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu; nao wanitafuta roho yangu waiondoe. 15 Bwana akamwambia, Enenda, urudi njia ya jangwa la Dameski; ukifika, mtie mafuta Hazaeli awe mfalme wa Shamu. 16 Na Yehu mwana wa Nimshi mtie mafuta awe mfalme wa Israeli; na Elisha mwana wa Shafati wa Abel-Mehola mtie mafuta awe nabii mahali pako. 17 Na itakuwa atakayeokoka na upanga wa Hazaeli, Yehu atamwua; na atakayeokoka na upanga wa Yehu, Elisha atamwua. 18 Pamoja na hayo nitajisazia katika Israeli watu elfu saba, kila goti lisilomwinamia Baali, na kila kinywa kisichombusu. 19 Basi, akaondoka huko, akamkuta Elisha mwana wa Shafati, aliyekuwa akilima, mwenye jozi za ng'ombe kumi na mbili mbele yake, na yeye mwenyewe alikuwa pamoja na lile la kumi na mbili. Eliya akapita karibu naye, akatupa vazi lake juu yake. 20 Naye akawaacha ng'ombe, akamfuata Eliya mbio, akasema, Nipe ruhusa, nakuomba, nimbusu baba yangu na mama yangu, kisha mimi nitakufuata. Akamwambia, Enenda, urudi; ni nini niliyokutendea? 21 Akarudi akiacha kumfuata, akatwaa lile jozi la ng'ombe, akawachinja, akatokosa nyama zao kwa ile miti ya ng'ombe, akawapa watu, wakala. Kisha akainuka, akamfuata Eliya, akamhudumia.

1 Wafalme 20

1 Basi, Ben-hadadi mfalme wa Shamu akakusanya jeshi lake lote; nao walikuwapo wafalme thelathini na wawili pamoja naye, na farasi, na magari: akakwea akauhusuru Samaria, akaupiga vita. 2 Akatuma wajumbe kwa Ahabu mfalme wa Israeli, mjini, akamwambia, Ndivyo asemavyo Ben-hadadi. 3 Fedha yako na dhahabu yako ni zangu mimi; na wakezo na wanao, walio wema, ni wangu. 4 Mfalme wa Israeli akajibu, akasema, Ni kama ulivyosema, bwana wangu, mfalme; mimi ni wako, na vyote nilivyo navyo. 5 Wajumbe wakarudi tena, wakasema, Ndivyo asemavyo Ben-hadadi, Hakika nimetuma kwako kusema, Fedha yako, na dhahabu yako, na wake zako, na wanao, utanitolea mimi; 6 lakini kesho kama wakati huu nitatuma kwako watumwa wangu, ili watazame-tazame nyumba yako na nyumba za watumwa wako; na itakuwa kila kipendezacho machoni pako watakitia mikononi mwao,na kukichukua. 7 Ndipo mfalme wa Israeli, akawaita wazee wote wa nchi, akasema, Angalieni, nawaomba, mwone, kwamba huyu ataka madhara; maana ametuma kwangu kutaka wake zangu na watoto wangu; na fedha yangu na dhahabu yangu, sikumkatalia. 8 Wakamwambia wazee wote na watu wote, Usisikie, wala usikubali. 9 Kwa hiyo akawaambia wale wajumbe wa Ben-hadadi, Mwambieni bwana wangu mfalme, Kila uliyotuma kumtakia mtumwa wako kwanza, nitafanya, ila neno hili siwezi kulifanya. Basi wajumbe wakaenda zao, wakamrudishia maneno hayo. 10 Ndipo Ben-hadadi akatuma kwake, akasema, Miungu wanifanyie hivi na kuzidi, yakiwa mavumbi ya Samaria yatatosha makonzi ya watu wote walio miguuni pangu. 11 Mfalme wa Israeli akajibu, akasema, Mwambieni, Avaaye asijisifu kama avuaye. 12 Ikawa, Ben-hadadi alipolisikia neno hilo, naye alikuwa akinywa, yeye na wafalme, mabandani, aliwaambia watumwa wake, Jipangeni. Wakajipanga juu ya mji. 13 Na tazama, nabii akamjia Ahabu mfalme wa Israeli, akasema, Bwana asema hivi, Je! Umeona makutano haya yote walio wengi? Angalia, nitawatia leo mkononi mwako; nawe utajua ya kuwa ndimi Bwana. 14 Ahabu akanena, Kwa nani? Akasema, Bwana asema hivi, Kwa vijana wa maliwali wa majimbo. Ndipo akanena, Ni nani atakayepanga vita? Naye akajibu, Ni wewe. 15 Ndipo akawaandika vijana wa maliwali wa majimbo, nao walikuwa mia mbili thelathini na wawili; kisha baada ya hao akawaandika watu wote, wana wa Israeli wote, nao walikuwa elfu saba. 16 Wakatoka wakati wa adhuhuri. Lakini Ben-hadadi alikuwa akinywa hata kulewa mabandani, yeye na wale wafalme thelathini na wawili waliomsaidia. 17 Wakatoka wale vijana wa maliwali wa majimbo wakitangulia; na Ben-hadadi akatuma watu, nao wakamwambia, Wako watu wametoka katika Samaria. 18 Akasema, Kwamba wametoka kwa amani, wakamateni wa hai; au kwamba wametoka kwa vita, wakamateni wa hai. 19 Basi wakatoka mjini hao vijana wa maliwali wa majimbo, na jeshi nyuma yao. 20 Wakapiga kila mmoja mtu wake; Washami wakakimbia, na Israeli wakawafuatia; Ben-hadadi mfalme wa Shamu akaokoka amepanda farasi, pamoja na wapandao farasi. 21 Mfalme wa Israeli akatoka, akawapiga farasi na magari, akawapiga Washami pigo kubwa. 22 Naye yule nabii akamjia mfalme wa Israeli, akamwambia, Enenda, kusanya nguvu zako, ujue, na kuangalia ufanyavyo; kwa maana mwakani mfalme wa Shamu atakuja juu yako. 23 Basi watumwa wake mfalme wa Shamu wakamwambia, Mungu wao ni mungu wa milima; ndiyo sababu ya kutushinda sisi; lakini na tupigane nao katika nchi tambarare, na hakika tutawashinda wao. 24 Ufanye neno hili; uwaondoe hao wafalme, kila mtu atoke mahali pake, ukaweke majemadari mahali pao. 25 Kisha ujihesabie jeshi, kama jeshi lililokupotea, farasi kwa farasi na gari kwa gari; nasi tutapigana nao katika nchi tambarare, na bila shaka tutawashinda. Akaisikiliza sauti yao, akafanya kama hivyo. 26 Basi ikawa mwakani, Ben-hadadi akawahesabu Washami, akakwea mpaka Afeki ili apigane na Israeli. 27 Wana wa Israeli nao wakahesabiwa, wakapewa vyakula, wakaenda kupigana nao; wakatua wana wa Israeli mbele yao kama vikundi viwili vya wana-mbuzi; bali Washami wakaijaza nchi. 28 Akaja yule mtu wa Mungu, akamwambia mfalme wa Israeli, akasema, Bwana asema hivi, Kwa sababu Washami wamesema, Bwana ni Mungu wa milima wala si Mungu wa nchi tambarare; basi nitawatia makutano haya yote walio wengi mkononi mwako, nanyi mtajua ya kuwa ndimi Bwana. 29 Wakatua kuelekeana muda wa siku saba. Ikawa siku ya saba vikapangwa vita; wana wa Israeli wakawapiga miongoni mwa Washami siku moja watu mia elfu waendao kwa miguu. 30 Lakini waliosalia wakakimbia mpaka Afeki, mjini; na ukuta ukaanguka juu ya watu ishirini na saba elfu waliosalia. Ben-hadadi naye akakimbia, akaingia mjini, katika chumba cha ndani. 31 Watumwa wake wakamwambia, Angalia sasa, tumesikia ya kuwa wafalme wa nyumba ya Israeli ni wafalme wenye rehema; tafadhali, tuvae magunia viunoni, na kamba vichwani, tumtokee mfalme wa Israeli; labda atakuokoa roho yako. 32 Basi wakajifungia magunia viunoni, na kamba vichwani, wakamjia mfalme wa Israeli, wakasema, Mtumwa wako Ben-hadadi asema Roho yangu, nakusihi, iishi. Akasema, Je! Yu hai bado? Ni ndugu yangu yeye. 33 Wale watu wakaangalia sana, wakafanya haraka kulishika neno hilo kama ni nia yake, wakasema, Ndugu yako, Ben-hadadi. Akasema, Haya! Nendeni mkamlete. Ndipo Ben-hadadi akamtokea, naye akampandisha garini. 34 Na Ben-hadadi akamwambia, Miji ile baba yangu aliyomnyang'anya baba yako nitairudisha; nawe utajifanyia njia huko Dameski, kama baba yangu aliyoifanya huko Samaria. Ahabu akasema, Nami nitakuacha kwa mapatano haya. Akafanya mapatano naye, akamwacha. 35 Basi, mtu mmoja wa wana wa manabii akamwambia mwenzake kwa neno la Bwana, Nipige, nakusihi. Akakataa yule kumpiga. 36 Akamwambia, Kwa sababu hukuisikiliza sauti ya Bwana, angalia, mara ukitoka kwangu simba atakuua. Na mara alipotoka kwake, simba alimwona, akamwua. 37 Ndipo akaona mtu mwingine, akasema, Nipige, nakusihi. Yule mtu akampiga, hata kumpiga na kumtia jeraha. 38 Basi yule nabii akaenda akamngoja mfalme njiani, amejibadilisha kwa kilemba juu ya macho yake. 39 Ikawa mfalme alipopita, alimwita mfalme; akasema, Mtumwa wako aliingia katikati ya pigano; na tazama, mtu mmoja akanigeukia akaniletea mtu, akaniambia, Umlinde mtu huyu; akipotea kwa njia yo yote, roho yako itakuwa mahali pa roho yake, au utatoa talanta ya fedha. 40 Ikawa mtumishi wako alipokuwa akitenda haya na haya, yule akaenda zake. Mfalme wa Israeli akamwambia, Ndivyo itakavyokuwa hukumu yako; umejihukumu mwenyewe. 41 Akafanya haraka akakiondoa kilemba machoni mwake, mfalme wa Israeli akamtambua kuwa ni mmoja wao manabii. 42 Akamwambia, Bwana asema hivi, Kwa sababu umemwachilia atoke mkononi mwako mtu niliyemweka ili aangamizwe kabisa, roho yako itakuwa mahali pa roho yake, na watu wako mahali pa watu wake. 43 Mfalme wa Israeli akaenda nyumbani kwake na moyo mzito, mwenye hasira, akaja Samaria.

1 Wafalme 21

1 Ikawa baada ya hayo, Nabothi Myezreeli alikuwa na shamba la mizabibu katika Yezreeli, karibu na nyumba ya kifalme ya Ahabu mfalme wa Samaria. 2 Ahabu akasema na Nabothi, akamwambia, Nipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, maana ni karibu na nyumba yangu; nami nitakupa badala yake shamba la mizabibu lililo zuri zaidi; au ukipenda, nitakupa fedha sawasawa na thamani yake. 3 Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu. 4 Basi Ahabu akaenda nyumbani kwake, ana moyo mzito, tena amekasirika, kwa sababu ya neno lile aliloambiwa na Nabothi Myezreeli, akisema, Sitakupa urithi wa baba zangu. Akajilaza kitandani pake, akageuza uso wake, akakataa kula. 5 Lakini Yezebeli mkewe akamwendea, akamwambia, Kwa nini roho yako ina huzuni hata usile chakula? 6 Akamwambia, Kwa sababu nimesema na Nabothi Myezreeli, nikamwambia, Unipe shamba lako la mizabibu kwa fedha, au, ukipenda, nitakupa shamba la mizabibu lingine badala yake. Akajibu, Sitakupa shamba langu la mizabibu. 7 Yezebeli mkewe akamwambia, Je! Sasa wewe unaumiliki ufalme wa Israeli? Ondoka, ule chakula, moyo wako ufurahi; mimi nitakupa shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli. 8 Basi, akaandika nyaraka kwa jina la Ahabu, akazitia muhuri yake, akazipeleka zile nyaraka kwa wazee, na kwa watu wenye nguvu waliokuwa katika mji wake, waliokaa pamoja na Nabothi. 9 Akaandika katika zile nyaraka, akasema, Pigeni mbiu ya watu kufunga, mkamweke Nabothi juu mbele ya watu, 10 mkainue watu wawili, watu wasiofaa, ili wamshitaki, na kumshuhudia, kunena, Umemtukana Mungu na mfalme. Kisha mchukueni nje, mkampige kwa mawe, ili afe. 11 Wale wazee wa mji wake, na walio wenye nguvu waliokaa mjini mwake, wakafanya kama Yezebeli alivyowaagiza, kama ilivyoandikwa katika nyaraka alizowapelekea. 12 Wakapiga mbiu ya watu kufunga, wakamweka Nabothi juu mbele ya watu. 13 Na hao watu wawili, watu wasiofaa, wakaingia, wakaketi mbele yake; wale watu wasiofaa wakamshuhudia Nabothi mbele ya watu, wakasema, Nabothi amemtukana Mungu na mfalme. Ndipo wakamchukua nje ya mji, wakampiga kwa mawe hata akafa. 14 Wakampelekea Yezebeli habari, wakasema, Nabothi amepigwa kwa mawe, amekufa. 15 Ikawa Yezebeli aliposikia ya kwamba Nabothi amepigwa kwa mawe na kufa, Yezebeli akamwambia Ahabu, Inuka, ulitamalaki shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli, alilokataa kukupa kwa fedha, maana Nabothi hako hai, lakini amekufa. 16 Ikawa Ahabu aliposikia ya kwamba Nabothi amekufa, akaondoka, alitelemkie shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli, ili alitamalaki. 17 Neno la Bwana likamjia Eliya Mtishbi, kusema, 18 Ondoka, ushuke, ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli, akaaye katika Samaria; yuko katika shamba la mizabibu la Nabothi, ndiko alikoshukia ili alitamalaki. 19 Ukamwambie, ukisema, Bwana asema hivi, Je! Umeua, ukatamalaki? Nawe utamwambia, kusema, Bwana asema hivi, Mahali pale mbwa walipoiramba damu ya Nabothi, mbwa watairamba na damu yako, naam, damu yako. 20 Ahabu akamwambia Eliya, Je! Umenipata, ewe adui yangu? Akamwambia, Nimekupata, kwa sababu umejiuza utende yaliyo mabaya machoni pa Bwana. 21 Angalia, nitaleta mabaya juu yako; nami nitakuangamiza kabisa, nitamkatia Ahabu kila mume, aliyefungwa na aliyeachwa katika Israeli. 22 Kisha nitaifanya nyumba yako iwe kama nyumba ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na kama nyumba ya Baasha mwana wa Ahiya, kwa ajili ya chukizo ulilonichukiza, hata kunighadhibisha, ukawakosesha Israeli. 23 Tena Bwana alinena habari za Yezebeli, akisema, Mbwa watamla Yezebeli katika kiwanja cha Yezreeli. 24 Mtu wa nyumba ya Ahabu afaye mjini, mbwa watamla, na yeye afaye mashambani ndege wa angani watamla. 25 (Lakini hapakuwa na mtu kama Ahabu, aliyejiuza atende maovu machoni pa Bwana ambaye Yezebeli mkewe alimchochea. 26 Akachukiza mno, kwa kuzifuata sanamu sawasawa na yote waliyoyafanya Waamori, Bwana aliowafukuza mbele ya wana wa Israeli.) 27 Ikawa, Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa magunia mwilini mwake, akafunga, akajilaza juu ya magunia, akaenda kwa upole. 28 Neno la Bwana likaja kwa Eliya Mtishbi, kusema, 29 Huoni jinsi Ahabu alivyojidhili mbele yangu? Basi kwa sababu amejidhili mbele yangu, sitayaleta yale mabaya katika siku zake; ila katika siku za mwanawe nitayaleta mabaya hayo juu ya nyumba yake.

1 Wafalme 22

1 Wakakaa miaka mitatu pasipo vita kati ya Shamu na Israeli. 2 Ikawa, mwaka wa tatu Yehoshafati mfalme Wa Yuda akamshukia mfalme wa Israeli. 3 Mfalme wa Israeli akawaambia watumishi wake, Je! Hamjui ya kuwa Ramoth-Gileadi ni yetu? Nasi tumenyamaza tusiitwae mkononi mwa mfalme wa Shamu? 4 Akamwambia Yehoshafati, Je! Utakwenda nami tupigane na Ramoth-gileadi? Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli, Mimi ni kama wewe, na watu wangu ni kama watu wako na farasi zangu ni kama farasi zako. 5 Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli, Uulize leo, nakusihi, kwa neno la Bwana. 6 Ndipo mfalme wa Israeli akawakusanya pamoja manabii, kama watu mia nne. Akawaambia Je! Niende juu ya Ramoth-Gileadi kuupiga vita, au ninyamaze? Wakasema Kwea; kwa kuwa Bwana atautia mkononi mwa mfalme. 7 Lakini Yehoshafati akasema, Je! Hayupo hapa nabii wa Bwana tena, ili tumwulize yeye? 8 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Yupo mtu mmoja, ambaye tungeweza kumwuliza Bwana kwa yeye, yaani Mikaya mwana wa Imla; lakini namchukia; kwa sababu hanibashirii mema, ila mabaya. Yehoshafati akasema, La! Mfalme asiseme hivi. 9 Ndipo mfalme wa Israeli akamwita akida, akamwambia, mlete hima Mikaya mwana wa Imla. 10 Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wakikaa kila mtu katika kiti chake cha enzi, wamevaa mavazi yao, katika sakafu langoni pa Samaria; na manabii wote wakafanya unabii mbele yao. 11 Na Zedekia mwana wa Kenaana akajifanyia pembe za chuma, akasema, Bwana asema hivi, Kwa hizo utawasukuma Washami, hata waharibike. 12 Na manabii wote wakasema hivyo kwa unabii, wakisema, Kwea Ramoth-Gileadi, ukafanikiwe; kwa kuwa Bwana atautia mkononi mwa mfalme. 13 Na yule mjumbe, aliyekwenda kumwita Mikaya, akamwambia, akasema, Angalia sasa, maneno ya manabii kwa kinywa kimoja husema mema kwa mfalme; neno lako na liwe, nakusihi, kama neno la mmojawapo wao, ukaseme mema. 14 Mikaya akasema, Kama Bwana aishivyo, neno lile Bwana aniambialo, ndilo nitakalolinena. 15 Na alipokuja kwa mfalme, mfalme alimwambia, Je! Mikaya, tuende Ramoth-Gileadi kupiga vita, au tunyamaze? Akamwambia, Kwea, ufanikiwe; kwa kuwa Bwana atautia mkononi mwa mfalme. 16 Mfalme akamwambia, Mara ngapi nikuapishe usiniambie neno ila yaliyo kweli, kwa jina la Bwana? 17 Akasema, Naliwaona Waisraeli wote wametawanyika milimani, kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana akasema, Hawa hawana bwana; na warudi kila mtu nyumbani kwake kwa amani. 18 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Je! Sikukuambia, hatanibashiria mema, ila mabaya? 19 Mikaya akasema, Sikia basi neno la Bwana; Nalimwona Bwana ameketi katika kiti chake cha enzi, na jeshi lote la mbinguni wamesimama upande wa mkono wake wa kuume na wa kushoto. 20 Bwana akasema, Ni nani atakayemdanganya Ahabu, ili akwee Ramoth-Gileadi akaanguke? Basi huyu akasema hivi; na huyu hivi. 21 Akatoka pepo, akasimama mbele za Bwana, akasema, Mimi nitamdanganya. 22 Bwana akamwambia, Jinsi gani? Akasema, Nitaondoka, na kuwa pepo wa uongo kinywani mwa manabii wake wote. Akasema, Utamdanganya, na kudiriki pia; ondoka ukafanye hivyo. 23 Basi angalia, Bwana ametia pepo wa uongo kinywani mwa manabii wako hawa wote; naye Bwana amenena mabaya juu yako. 24 Ndipo akakaribia Zedekia, mwana wa Kenaana, akampiga Mikaya kofi la shavu, akasema, Roho ya Bwana alitokaje kwangu ili aseme na wewe? 25 Mikaya akamwambia, Angalia, utaona siku ile utakapoingia katika chumba cha ndani ili ujifiche. 26 Mfalme wa Israeli akasema, Mchukueni Mikaya, mkamrudishe kwa Amoni mkuu wa mji na kwa Yoashi mwana wa mfalme; 27 mkaseme, Mfalme asema hivi, Mtieni mtu huyu gerezani, mkamlishe kwa chakula cha shida, na maji ya shida, hata nitakaporudi kwa amani. 28 Mikaya akasema, Ukirudi kabisa kwa amani, Bwana hakusema kwa mimi. Akasema, Sikieni, enyi watu wote. 29 Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda wakakwea mpaka Ramoth-Gileadi. 30 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Nitajibadilisha, na kuingia vitani; lakini wewe uvae mavazi yako. Mfalme wa Israeli akajibadilisha, akaingia vitani. 31 Basi mfalme wa Shamu alikuwa amewaamuru wakuu wa magari yake thelathini na wawili, akisema, Msipigane na mdogo wala mkuu, ila na mfalme wa Israeli peke yake. 32 Ikawa wakuu wa magari walipomwona Yehoshafati, wakasema, Huyo ndiye mfalme wa Israeli Wakageuka juu yake ili wapigane naye; naye Yehoshafati akapiga ukelele. 33 Ikawa, wakuu wa magari walipoona ya kuwa siye mfalme wa Israeli, wakageuka nyuma wasimfuate. 34 Mtu mmoja akavuta upinde kwa kubahatisha, akampiga mfalme wa Israeli mahali pa kuungana mavazi yake ya chuma; kwa hiyo akamwambia mwendesha gari lake, Geuza mkono wako, unichukue kutoka katika majeshi; kwa kuwa nimejeruhiwa sana. 35 Pigano likazidi siku ile; mfalme akategemezwa garini mwake, kinyume cha Washami, hata jioni akafa; damu ikatoka katika jeraha yake ndani ya gari. 36 Ikapigwa mbiu jeshini, jua likichwa, kusema, Kila mtu aende mjini kwake, na kila mtu shambani kwake. 37 Hivyo akafa mfalme, akachukuliwa Samaria, wakamzika mfalme huko Samaria. 38 Wakaliosha gari penye birika la Samaria, na mbwa wakaramba damu yake; (basi ndipo walipooga makahaba); sawasawa na neno la Bwana alilolinena. 39 Na mambo yote ya Ahabu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, na nyumba ya pembe aliyoijenga, na miji yote aliyoijenga, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 40 Basi Ahabu akalala na baba zake; na Ahazia mwanawe akatawala mahali pake. 41 Yehoshafati mwana wa Asa alianza kutawala juu ya Yuda, katika mwaka wa nne wa Ahabu mfalme wa Israeli. 42 Yehoshafati alikuwa mwenye miaka thelathini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka ishirini na mitano huko Yerusalemu. Na jina la mamaye aliitwa Azuba binti Shilhi. 43 Akaiendea njia yote ya Asa babaye; wala hakugeuka, akifanya yaliyo mema machoni pa Bwana. Lakini mahali pa juu hapakuondolewa; watu wakaendelea kutoa dhabihu wakafukiza uvumba katika mahali pa juu. 44 Yehoshafati akafanya amani na mfalme wa Israeli. 45 Na mambo yote ya Yehoshafati yaliyosalia, na uthabiti alioufanya, na jinsi alivyopiga vita, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 46 Tena mahanithi waliosalia, hao waliosalia siku za Asa baba yake, akawaondoa katika nchi. 47 Wala hapakuwa na mfalme katika Edomu; naibu alikuwa ndiye mfalme. 48 Yehoshafati akafanya merikebu za Tarshishi ziende Ofiri kuchukua dhahabu; walakini hazikuenda; kwa maana merikebu zilivunjika huko Esion-geberi. 49 Ndipo Ahazia mwana wa Ahabu akamwambia Yehoshafati, Watumishi wangu na waende pamoja na watumishi wako merikebuni. Lakini Yehoshafati hakukubali. 50 Basi Yehoshafati akalala na babaze, akazikwa pamoja na babaze mjini mwa Daudi baba yake; na Yehoramu mwanawe akatawala mahali pake. 51 Ahazia mwana wa Ahabu alianza kutawala juu ya Israeli huko Samaria, katika mwaka wa kumi na saba wa Yehoshafati mfalme wa Yuda, akatawala miaka miwili juu ya Israeli. 52 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, akaiendea njia ya babaye, na njia ya mamaye, na njia ya Yeroboamu mwana wa Nebati, aliyewakosesha Israeli. 53 Akamtumikia Baali, akamwabudu, akamghadhibisha Bwana, Mungu wa Israeli, kwa mfano wa mambo yote aliyoyafanya baba yake.

2 Wafalme 1

1 Ikawa, baada ya kufa kwake Ahabu, Moabu wakawaasi Israeli. 2 Na Ahazia akaanguka katika dirisha la chumba chake orofani, katika Samaria, akaugua; akatuma wajumbe, akawaambia, Enendeni mkaulize kwa Baal-zebubu, mungu wa Ekroni, kwamba nitapona ugonjwa huu. 3 Lakini malaika wa Bwana akamwambia Eliya Mtishbi, Ondoka, uende ukaonane na wale wajumbe wa mfalme wa Samaria, ukawaambie, Je! Ni kwa sababu hapana Mungu katika Israeli, hata mnakwenda kuuliza kwa Baal-zebubu, mungu wa Ekroni? 4 Basi sasa, Bwana asema hivi, Hutashuka katika kile kitanda ulichokipanda, bali hakika utakufa. Eliya akaondoka. 5 Wale wajumbe wakarudi, na mfalme akawaambia, Mbona mmerudi? 6 Wakamwambia, Mtu alitokea, akaonana nasi, akatuambia, Enendeni, rudini kwa mfalme yule aliyewatuma, mkamwambie, Bwana asema hivi Je! Ni kwa sababu hapana Mungu katika Israeli, hata mnakwenda kuuliza kwa Baal-zebubu, mungu wa Ekroni? Basi kwa ajili ya hayo hutashuka katika kile kitanda ulichokipanda, bali hakika utakufa. 7 Akawaambia, Je! Mtu yule aliyetokea, akaonana nanyi, akawaambia maneno hayo, alikuwa mtu wa namna gani? 8 Wakamwambia, Alikuwa amevaa vazi la manyoya, tena amejifunga shuka ya ngozi kiunoni mwake. Naye akasema, Ndiye yule Eliya Mtishbi. 9 Ndipo mfalme akatuma akida wa askari hamsini pamoja na hamsini wake, wamwendee Eliya. Akamwendea, na tazama, ameketi juu ya kilima. Akamwambia, Ewe mtu wa Mungu, mfalme asema, Shuka. 10 Eliya akajibu, akamwambia yule akida wa hamsini, Ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, na ushuke moto kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na hamsini wako. Moto ukashuka, ukamteketeza, yeye na hamsini wake. 11 Akatuma tena akida wa hamsini mwingine pamoja na hamsini wake, wamwendee. Akajibu, akamwambia, Ewe mtu wa Mungu, mfalme asema, Shuka upesi. 12 Eliya akajibu, akamwambia, Ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, na ushuke moto kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na hamsini wako. Moto wa Mungu ukashuka kutoka mbinguni, ukamteketeza, yeye na hamsini wake. 13 Tena akatuma akida wa hamsini wa tatu, pamoja na hamsini wake. Yule akida wa hamsini wa tatu akapanda, akaenda akapiga magoti mbele ya Eliya, akamsihi sana, akamwambia, Ee mtu wa Mungu, nakusihi, roho yangu, na roho za watumishi wako hawa hamsini, ziwe na thamani machoni pako. 14 Tazama, moto ulishuka kutoka mbinguni, ukawateketeza wale akida wa hamsini wawili wa kwanza pamoja na hamsini wao; laiti sasa roho yangu na iwe na thamani machoni pako. 15 Malaika wa Bwana akamwambia Eliya, Shuka pamoja naye; usimwogope. Akaondoka, akashuka pamoja naye hata kwa mfalme. 16 Akamwambia, Bwana asema hivi, Kwa kuwa umetuma wajumbe waulize kwa Baal-zebubu, mungu wa Ekroni, je! Ni kwa sababu hapana Mungu katika Israeli, uulize neno lake? Kwa hiyo hutashuka katika kile kitanda ulichokipanda, bali hakika utakufa. 17 Basi akafa, sawasawa na neno la Bwana alilolinena Eliya. Na Yoramu alianza kutawala mahali pake katika mwaka wa pili wa Yehoramu mwana wa Yehoshafati mfalme wa Yuda; kwa kuwa yeye hakuwa na mwana. 18 Na mambo yote yaliyosalia aliyoyafanya Ahazia, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli?

2 Wafalme 2

1 Ikawa, hapo Bwana alipopenda kumpandisha Eliya mbinguni kwa upepo wa kisulisuli, Eliya alitoka Gilgali pamoja na Elisha. 2 Eliya akamwambia Elisha, Tafadhali, kaa hapa; maana Bwana amenituma niende mpaka Betheli. 3 Elisha akasema, Kama Bwana aishivyo, na roho yako iishivyo, sitakuacha, Basi wakashuka mpaka Betheli. Basi wana wa manabii, waliokuwako Betheli, wakatoka kuonana na Elisha, wakamwambia, Je! Unajua ya kuwa Bwana atamwondoa bwana wako leo, asiwe mkubwa wako? Akasema, Naam, najua; nyamazeni. 4 Eliya akamwambia, Tafadhali, kaa hapa, Elisha; maana Bwana amenituma niende mpaka Yeriko. Akasema, Kama Bwana aishivyo, na roho yako iishivyo, sitakuacha. Nao wakafika Yeriko. 5 Basi wana wa manabii, waliokuwako Yeriko, wakamkaribia Elisha, wakamwambia, Je! Unajua ya kuwa Bwana atamwondoa bwana wako leo, asiwe mkubwa wako? Akajibu, Naam, najua, nyamazeni. 6 Eliya akamwambia, Tafadhali kaa hapa; maana Bwana amenituma niende mpaka Yordani. Akasema, Kama Bwana aishivyo, na roho yako iishivyo, sitakuacha. Wakaendelea mbele wote wawili. 7 Basi watu hamsini wa wale wana wa manabii wakaenda wakasimama, kuwakabili kwa mbali; na hao wawili wakasimama karibu na Yordani. 8 Eliya akalitwaa vazi lake la juu, akalikunja, akayapiga maji, yakagawanyika huku na huku, na hao wawili wakavuka pakavu. 9 Hata ikawa, walipokwisha kuvuka, Eliya akamwambia Elisha, Omba kwangu lo lote utakalo nikutendee, kabla sijaondolewa kwako. Elisha akasema, Nakuomba, sehemu maradufu ya roho yako na iwe juu yangu. 10 Akasema, Umeomba neno gumu; lakini, ukiniona nitakapoondolewa kwako, utalipata; la hukuniona, hulipati. 11 Ikawa, walipokuwa wakiendelea mbele na kuongea, tazama! Kukatokea gari la moto, na farasi wa moto, likawatenga wale wawili; naye Eliya akapanda mbinguni kwa upepo wa kisulisuli. 12 Naye Elisha akaona, akalia, Baba yangu, baba yangu, gari la Israeli na wapanda farasi wake! Asimwone tena kabisa; akashika mavazi yake mwenyewe, akayararua vipande viwili. 13 Kisha akaliokota lile vazi la Eliya lililomwangukia, akarudi, akasimama katika ukingo wa Yordani. 14 Akalitwaa lile vazi la Eliya lililomwangukia, akayapiga maji, akasema, Yuko wapi Bwana, Mungu wa Eliya? Naye alipoyapiga maji, yakagawanyika huku na huku, Elisha akavuka. 15 Na hao wana wa manabii, waliokuwako Yeriko wakimkabili, walipomwona, walisema, Roho ya Eliya inakaa juu ya Elisha. Wakaja kuonana naye, wakainama kifudifudi mbele yake. 16 Wakamwambia, Angalia, wako hapa pamoja nasi watumishi wako watu hamsini walio hodari; waende, twakuomba, wamtafute bwana wako; isiwe labda roho ya Bwana imemtwaa na kumtupa juu ya mlima mmoja, au katika bonde moja. Akasema, Msiwatume. 17 Wakamsisitiza hata akaona haya, akasema, Haya! Watumeni. Basi wakatuma watu hamsini; nao wakatafuta siku tatu, wasimwone. 18 Wakamrudia, alipokuwa anakawia Yeriko; akawaambia, Je! Mimi sikuwaambia, Msiende? 19 Watu wa mjini wakamwambia Elisha, Angalia, twakusihi, mahali pa mji huu ni pazuri, kama bwana wangu aonavyo; lakini maji yake hayafai, na nchi huzaa mapooza. 20 Akasema, Nileteeni chombo kipya, mtie chumvi ndani yake. Wakamletea. 21 Akatoka akaenda mpaka chemchemi ya maji, akatupa ile chumvi humo ndani, akasema, Bwana asema hivi, Nimeyaponya maji haya; hakutatoka huko tena kufa wala kuzaa mapooza. 22 Hivyo yale maji yakapona hata leo, sawasawa na neno la Elisha alilolinena. 23 Akakwea kutoka huko mpaka Betheli; naye alipokuwa akienda njiani, wakatoka vijana katika mji, wakamfanyizia mzaha, wakamwambia, Paa wewe mwenye upaa! Paa wewe mwenye upaa! 24 Akatazama nyuma akawaona, akawalaani kwa jina la Bwana. Wakatoka dubu wawili wa kike mwituni, wakawararua vijana arobaini na wawili miongoni mwao. 25 Akatoka huko akaenda mlima wa Karmeli, na toka huko akarudi mpaka Samaria.

2 Wafalme 3

1 Basi Yoramu mwana wa Ahabu alianza kutawala juu ya Israeli huko Samaria katika mwaka wa kumi na nane wa Yehoshafati mfalme wa Yuda ,akatawala miaka kumi na miwili. 2 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana; ila si kama baba yake na kama mama yake; maana akaiondoa ile nguzo ya Baali aliyoifanya baba yake. 3 Pamoja na hayo alishikamana na dhambi za Yeroboamu mwana wa Nebati, ambazo kwa hizo aliwakosesha Israeli; wala hakuziacha. 4 Basi Mesha, mfalme wa Moabu, alikuwa mfuga kondoo; naye alikuwa akimlipa mfalme wa Israeli sufu ya wana-kondoo elfu mia, na ya kondoo waume elfu mia. 5 Lakini ikawa, Ahabu alipokufa, mfalme wa Moabu akamwasi mfalme wa Israeli. 6 Akatoka wakati ule ule mfalme Yoramu katika Samaria, akawahesabu Israeli wote. 7 Akaenda akatuma kwa Yehoshafati mfalme wa Yuda, akasema, Mfalme wa Moabu ameniasi; je! Utakwenda pamoja nami tupigane na Moabu? Akasema, Nitakwenda; mimi ni kama wewe, watu wangu ni kama watu wako, farasi zangu ni kama farasi zako. 8 Akauliza, Njia ipi tuiendee? Akajibu, Njia ya jangwa la Edomu. 9 Basi mfalme wa Israeli akaenda, na mfalme wa Yuda, na mfalme wa Edomu; wakazunguka mwendo wa siku saba; wala hapakuwa na maji kwa jeshi, wala kwa wanyama waliowafuata. 10 Mfalme wa Israeli akasema, Ole wetu! Kwani Bwana amewakutanisha hawa wafalme watatu, awaue mkononi mwa Moabu. 11 Lakini Yehoshafati akasema, Je! Hapana hapa nabii wa Bwana, ili tumwulize Bwana kwa yeye? Akajibu mtumishi mmoja wa mfalme wa Israeli, akasema, Yupo hapa Elisha mwana wa Shafati, aliyekuwa akimimina maji juu ya mikono yake Eliya. 12 Yehoshafati akasema, Neno la Bwana analo huyu. Basi mfalme wa Israeli, na Yehoshafati, na mfalme wa Edomu, wakamshukia. 13 Elisha akamwambia mfalme wa Israeli, Nina nini mimi nawe? Uende kwa manabii wa babayo, na manabii wa mamayo. Mfalme wa Israeli akamwambia, La, sivyo; kwa kuwa Bwana amewakutanisha hawa wafalme watatu, awaue mkononi mwa Moabu. 14 Elisha akasema, Kama Bwana wa majeshi aishivyo, ambaye nimesimama mbele zake, kama singemwangalia uso wake Yehoshafati mfalme wa Yuda, singekutazama, wala kuonana nawe. 15 Ila sasa niletee mpiga kinanda. Ikawa, mpiga kinanda alipokipiga, mkono wa Bwana ukamjia juu yake. 16 Akasema, Bwana asema hivi, Fanyeni bonde hili lijae mahandaki. 17 Kwa kuwa Bwana asema hivi, Hamutauona upepo, wala hamtaiona mvua, ila bonde hilo litajaa maji; nanyi mtakunywa, ninyi, na ng'ombe zenu, na wanyama wenu. 18 Na jambo hili ni jepesi machoni pa Bwana; pia atawatia Wamoabi mikononi mwenu. 19 Nanyi mtapiga kila mji wenye boma, na kila mji ulio mzuri, na kila mti mwema mtaukata, na chemchemi zote za maji mtaziziba, na kila mahali palipo pema mtapaharibu kwa mawe. 20 Ikawa asubuhi, wakati wa kutoa sadaka ya unga, tazama, maji yakaja kwa njia ya Edomu, hata nchi ikajaa maji. 21 Basi Wamoabi wote waliposikia ya kuwa wafalme hao wamekwea ili kupigana nao, walijikusanya pamoja, wote wawezao kuvaa silaha, na wenye umri zaidi, wakasimama mpakani. 22 Wakaamka asubuhi na mapema, na hilo jua likameta-meta juu ya maji, na Wamoabi wakayaona yale maji yaliyowaelekea kuwa ni mekundu kama damu. 23 Wakasema, Ndiyo damu hii; bila shaka hao wafalme wameharibika, wamepigana kila mtu na mwenziwe; basi sasa, enyi Wamoabi, nyara hizo! 24 Hata walipokuja matuoni kwa Israeli, Waisraeli wakainuka wakawapiga Wamoabi, hata wakakimbia mbele yao; wakaendelea wakiwapiga-piga Wamoabi hata kwao. 25 Wakaibomoa ile miji; wakatupa katika kila mahali palipo pema kila mtu jiwe lake, wakapajaza; wakaziziba chemchemi zote za maji, wakaikata miti yote iliyo mizuri; mpaka katika Kir-haresethi tu wakayasaza mawe yake; ila wenye kombeo wakauzunguka wakaupiga. 26 Naye mfalme wa Moabu alipoona ya kwamba ameshindwa vitani, alitwaa pamoja naye watu mia saba wenye kufuta panga ili wapenye hata kwa mfalme wa Edomu; wala hawakudiriki. 27 Ndipo akamtwaa mwanawe wa kwanza, yeye ambaye angetawala mahali pake, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa juu ya ukuta. Kukawa hasira kuu juu ya Israeli; basi wakatoka kwake, wakarudi kwenda nchi yao wenyewe.

2 Wafalme 4

1 Basi, mwanamke mmoja miongoni mwa wake za wana wa manabii alimlilia Elisha, akasema, Mtumishi wako mume wangu amekufa; nawe unajua ya kuwa mtumishi wako alikuwa mcha Bwana; na aliyemwia amekuja ili ajitwalie wana wangu wawili kuwa watumwa. 2 Elisha akamwambia, Nikufanyie nini? Niambie; una kitu gani nyumbani? Akasema, Mimi mjakazi wako sina kitu nyumbani, ila chupa ya mafuta. 3 Akasema, Nenda, ukatake vyombo huko nje kwa jirani zako wote, vyombo vitupu; wala usitake vichache. 4 Kisha uingie ndani, ukajifungie mlango wewe na wanao, ukavimiminie mafuta vyombo vile vyote; navyo vilivyojaa ukavitenge. 5 Basi akamwacha, akajifungia mlango yeye na wanawe; hao wakamletea vile vyombo, na yeye akamimina. 6 Ikawa, vilipokwisha kujaa vile vyombo, akamwambia mwanawe, Niletee tena chombo. Akamwambia, Hakuna tena chombo. Mafuta yakakoma. 7 Ndipo akaja akamwambia yule mtu wa Mungu. Naye akasema, Enenda ukayauze mafuta haya, uilipe deni yako; nayo yaliyosalia uyatumie wewe na watoto wako. 8 Hata ikawa siku moja, Elisha alikwenda Shunemu; na huko kulikuwa na mwanamke mmoja mwenye cheo; naye akamshurutisha aje ale chakula. Ikawa kila alipopita njia ile, huingia kula chakula. 9 Yule mwanamke akamwambia mumewe, Tazama, mimi naona ya kuwa mtu huyu apitaye kwetu mara kwa mara ni mtu mtakatifu wa Mungu. 10 Nakuomba, tumfanyie chumba kidogo ukutani; na ndani yake tumwekee kitanda, na meza, na kiti, na kinara cha taa; na itakuwa, atujiapo, ataingia humo. 11 Ikawa siku moja akafika huko, akaingia katika chumba kile akalala. 12 Akamwambia Gehazi mtumishi wake, Mwite yule Mshunami. Naye alipokwisha kuitwa, akasimama mbele yake. 13 Akamwambia, Sema naye sasa, Tazama, wewe umetutunza sana namna hii; utendewe nini basi? Je! Uombewe neno kwa mfalme, au kwa amiri wa jeshi? Yule mwanamke akamjibu, Mimi ninakaa katika watu wangu mwenyewe. 14 Akasema, Basi, atendewe nini? Gehazi akajibu, Hakika hana mwana, na mumewe ni mzee. 15 Akamwambia, Kamwite. Naye alipokwisha kuitwa, akasimama mlangoni. 16 Akasema, Panapo wakati huu mwakani, utamkumbatia mwana. Akasema, La! Bwana wangu, wewe mtu wa Mungu, usiniambie mimi mjakazi wako uongo. 17 Yule mwanamke akachukua mimba, akazaa mtoto mume wakati uo huo mwakani, kama Elisha alivyomwambia. 18 Hata yule mtoto alipokua, ikawa siku moja alitoka kwenda kwa baba yake kwenye wavunao. 19 Akamwambia baba yake, Kichwa changu! Kichwa changu! Naye akamwambia mtumishi wake, Mchukue kwa mama yake. 20 Akamchukua, akampeleka kwa mama yake, naye akakaa magotini mwake hata adhuhuri, kisha akafa. 21 Mamaye akapanda juu, akamlaza juu ya kitanda cha yule mtu wa Mungu, akamfungia mlango, akatoka. 22 Kisha akamwita mumewe, akasema, Tafadhali, uniletee mtu mmoja wa watumishi, na punda mmoja, ili nimwendee yule mtu wa Mungu kwa haraka, nikarudi tena. 23 Akasema, Kwa nini kumwendea leo? Sio mwandamo wa mwezi, wala sabato. Akasema, Si neno. 24 Akatandika punda, akamwambia mtumishi wake, Mwendeshe, twendelee mbele. Usinipunguzie mwendo, nisipokuambia. 25 Basi akaenda, akafika kwa yule mtu wa Mungu, katika mlima wa Karmeli. Ikawa, yule mtu wa Mungu alipomwona kwa mbali, akamwambia Gehazi mtumishi wake, Tazama, Mshunami yule kule. 26 Tafadhali piga mbio sasa kwenda kumlaki, ukamwambie, Hujambo? Mume wako hajambo? Mtoto hajambo? Akajibu, Hawajambo. 27 Naye alipofika kwa yule mtu wa Mungu kilimani, alimshika miguu. Gehazi akakaribia amwondoe; lakini mtu wa Mungu akamwambia, Mwache; maana roho yake ndani yake ina uchungu; na Bwana amenificha, wala hakuniambia. 28 Yule mwanamke akasema, Je! Naliomba mwana kwa bwana wangu? Mimi sikusema, Usinidanganye? 29 Ndipo Elisha akamwambia Gehazi, Jikaze viuno, ukachukue fimbo yangu mkononi mwako, ukaende zako; ukikutana na mtu, usimsalimu; na mtu akikusalimu, usimjibu; ukaweke fimbo yangu juu ya uso wa mtoto. 30 Na mama yake yule mtoto akasema, Kama Bwana aishivyo, na roho yako iishivyo, sitakuacha. Basi akaondoka, akamfuata. 31 Na Gehazi akawatangulia, akaiweka ile fimbo juu ya uso wa mtoto; lakini hapakuwa na sauti, wala majibu. Basi akarudi ili kumlaki, akamwambia, akisema, Mtoto hakuamka. 32 Basi Elisha alipofika nyumbani, tazama, mtoto amekwisha kufa, amelazwa kitandani pake. 33 Basi akaingia ndani, akajifungia mlango, yeye na yule mtoto wote wawili, akamwomba Bwana. 34 Akapanda juu ya kitanda, akajilaza juu ya mtoto, akaweka kinywa chake juu ya kinywa chake, na macho yake juu ya macho yake, na mikono yake juu ya mikono yake; akajinyosha juu yake; mwili wake yule mtoto ukaanza kupata moto. 35 Kisha akarudi, akatembea nyumbani, huko na huko mara moja; akapanda, akajinyosha juu yake; na yule mtoto akapiga chafya mara saba, na mtoto akafumbua macho yake. 36 Akamwita Gehazi, akasema, Mwite yule Mshunami. Basi akamwita. Na alipofika kwake, Elisha akasema, Haya! Mchukue mwanao. 37 Ndipo akaingia, akamwangukia miguu akainama mpaka nchi; kisha akamchukua mwanawe, akatoka. 38 Elisha akafika Gilgali tena; na kulikuwa na njaa katika nchi; na hao wana wa manabii walikuwa wakikaa mbele yake. Akamwambia mtumishi wake, Teleka sufuria kubwa, uwapikie wana wa manabii. 39 Na mmoja wao akaenda nje kondeni ili kuchuma mboga, akaona mtango-mwitu, akayachuma matango-mwitu, hata nguo yake ikawa imejaa, akaja akayapasua-pasua sufuriani; kwa maana hawakuyajua. 40 Basi wakawapakulia hao watu ili wale. Ikawa, walipokuwa katika kula chakula, wakapiga kelele, wakasema, Mauti imo sufuriani, Ee mtu wa Mungu. Wala hawakuweza kula. 41 Lakini yeye akasema, Leteni unga. Naye akautupa ndani ya sufuria; akasema, Wapakulie watu, ili wale. Wala hakikuwamo kitu kibaya sufuriani. 42 Tena, akaja mtu kutoka Baal-shalisha, akamletea mtu wa Mungu chakula cha malimbuko, mikate ishirini ya shayiri, na masuke mabichi ya ngano guniani. Akasema, Uwape watu, ili wale. 43 Na mtumishi wake akasema, Je! Niwaandikie hiki watu mia? Lakini akasema, Uwape watu, ili wale; kwa kuwa Bwana asema hivi, Watakula na kusaza. 44 Basi akawaandikia, nao wakala, wakasaza, sawasawa na neno la Bwana.

2 Wafalme 5

1 Basi Naamani, jemadari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake Bwana alikuwa amewapa Washami kushinda; tena alikuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa mwenye ukoma. 2 Na Washami walikuwa wametoka vikosi, wakachukua mfungwa mmoja kijana mwanamke kutoka nchi ya Israeli; naye akamhudumia mkewe Naamani. 3 Akamwambia bibi yake, Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake. 4 Mtu mmoja akaingia, akamwambia bwana wake, akasema, Yule kijana mwanamke aliyetoka nchi ya Israeli asema hivi na hivi. 5 Mfalme wa Shamu akasema, Haya! Basi, mimi nitampelekea mfalme wa Israeli waraka. Basi akaenda zake, akachukua mikononi mwake talanta kumi za fedha, na vipande vya dhahabu elfu sita, na mavazi kumi. 6 Akampelekea mfalme wa Israeli waraka ule, kusema, Waraka huu utakapokuwasilia, tazama, nimemtuma mtumishi wangu Naamani kwako, ili upate kumponya ukoma wake. 7 Ikawa, mfalme wa Israeli alipousoma waraka, alirarua mavazi yake, akasema, Je! Mimi ni Mungu, niue na kuhuisha, hata mtu huyu akanipelekea mtu nimponye ukoma wake? Fahamuni, basi, nakusihini, mwone ya kuwa mtu huyu anataka kugombana nami. 8 Ikawa, Elisha, yule mtu wa Mungu, aliposikia kwamba mfalme wa Israeli ameyararua mavazi yake, ndipo akatuma mtu kwa mfalme, akisema, Mbona umeyararua mavazi yako? Na aje sasa kwangu mimi, naye atajua ya kuwa yuko nabii katika Israeli. 9 Basi Naamani akaja na farasi wake na magari yake, akasimama mlangoni pa nyumba ya Elisha. 10 Naye Elisha akampelekea mjumbe, akisema, Enenda ukaoge katika Yordani mara saba, na nyama ya mwili wako itakurudia, nawe utakuwa safi. 11 Lakini Naamani akakasirika, akaondoka, akasema, Tazama, nalidhania, Bila shaka atatoka kwangu, na kusimama, na kuomba kwa jina la Bwana, Mungu wake, na kupitisha mkono wake mahali penye ugonjwa, na kuniponya mimi mwenye ukoma. 12 Je! Abana na Farpari, mito ya Dameski, si bora kuliko maji yote ya Israeli? Je! Siwezi kujiosha ndani yake, na kuwa safi? Akageuka, akaondoka kwa hasira. 13 Watumishi wake wakamkaribia, wakamwambia, wakasema, Baba yangu, kama yule nabii angalikuambia kutenda jambo kubwa, usingalilitenda? Je! Si zaidi basi, akikuambia, Jioshe, uwe safi? 14 Ndipo akashuka, akajichovya mara saba katika Yordani, sawasawa na neno lake yule mtu wa Mungu; nayo nyama ya mwili wake ikarudi ikawa kama nyama ya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi. 15 Akamrudia yule mtu wa Mungu, yeye na mafuatano yake yote. Akaja, akasimama mbele yake; akasema, Sasa tazama, najua ya kwamba hakuna Mungu duniani mwote, ila katika Israeli; basi nakuomba upokee mbaraka kwa mtumwa wako. 16 Lakini akasema, Kama Bwana aishivyo, ambaye nimesimama mbele yake, sipokei kitu. Akamshurutisha apokee; lakini akakataa. 17 Naamani akasema; Kama sivyo, lakini mtumwa wako na apewe mzigo wa udongo wa baghala wawili; kwa maana mtumwa wako hatatoa tena sadaka ya kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine, ila kwa Bwana. 18 Jambo hili Bwana amwachilie mtumwa wako; bwana wangu akiingia nyumbani mwa Rimoni ili aabudu humo, naye akitegemea mkononi mwangu, nami nikijiinama nyumbani mwa Rimoni, hapo ninapojiinama nyumbani mwa Rimoni, Bwana amwachilie mtumwa wako jambo hili. 19 Akamwambia, Enenda kwa amani Basi akamwondokea mbali kidogo. 20 Lakini Gehazi, mtumishi wa Elisha mtu wa Mungu, akasema, Tazama, bwana wangu amemwachilia huyo Naamani Mshami, asivipokee mikononi mwake vile vitu alivyovileta; kama Bwana aishivyo, mimi nitamfuata mbio, nipokee kitu kwake. 21 Basi Gehazi akamfuata Naamani. Naye Naamani, alipoona mtu apigaye mbio anakuja nyuma yake, alishuka garini amlaki, akasema, Je! Ni amani? 22 Akasema, Amani. Bwana wangu amenituma, kusema, Tazama, sasa hivi wamenijia kutoka milimani mwa Efraimu vijana wawili wa wana na manabii; uwape, nakuomba, talanta ya fedha, na mavazi mawili. 23 Naamani akasema, Uwe radhi, ukatwae talanta mbili. Akamshurutisha, akafunga talanta mbili za fedha ndani ya mifuko miwili, na mavazi mawili, akawatwika watumishi wake wawili; nao wakayachukua mbele yake. 24 Naye alipofika kilimani, alivitwaa mikononi mwao, akaviweka nyumbani; akawaacha wale watu kuondoka, nao wakaenda zao. 25 Lakini yeye akaingia, akasimama mbele ya bwana wake. Elisha akamwambia, Watoka wapi, Gehazi? Akanena, Mtumwa wako hakuenda mahali. 26 Akamwambia, Je! Moyo wangu haukuenda na wewe, hapo alipogeuka yule mtu katika gari ili akulaki? Je! Huu ndio wakati wa kupokea fedha, na kupokea mavazi, na mashamba ya mizeituni, na mizabibu, na kondoo, na ng'ombe, na watumwa, na wajakazi? 27 Basi ukoma wa Naamani utakushika wewe, na wazao wako hata milele. Naye akatoka usoni pake mwenye ukoma kama theluji.

2 Wafalme 6

1 Kisha, wana wa manabii wakamwambia Elisha, Angalia basi, mahali tukaapo mbele yako ni padogo kwetu. 2 Basi twende mpaka Yordani, twakuomba, tutwae huko kila mtu mti mmoja, ili tujifanyie huko mahali pa kukaa. Akajibu, Haya! Nendeni. 3 Mmoja wao akasema, Uwe radhi, basi nakusihi, uende pamoja na watumishi wako. Akajibu, Nitakwenda. 4 Basi, akaenda pamoja nao. Nao walipofika Yordani, wakakata miti. 5 Lakini mmojawapo alipokuwa katika kukata boriti, chuma cha shoka kikaanguka majini; akalia, akasema, Ole wangu! Bwana wangu, kwani kiliazimiwa kile. 6 Mtu wa Mungu akasema, Kilianguka wapi? Akamwonyesha mahali. Akakata kijiti, akakitupa pale pale, chuma kikaelea. 7 Akasema, Kiokote. Basi akanyosha mkono, akakitwaa. 8 Basi, mfalme wa Shamu alikuwa akifanya vita na Israeli. Akafanya mashauri na watumishi wake, akasema, Kituo changu kitakuwapo mahali fulani. 9 Yule mtu wa Mungu akapeleka habari kwa mfalme wa Israeli, kusema, Jihadhari, usipite mahali fulani; kwa sababu ndiko wanakoshukia Washami. 10 Mfalme wa Israeli akapeleka watu mpaka mahali pale alipoambiwa na yule mtu wa Mungu, na kuhadharishwa; akajiokoa nafsi yake, si mara moja, wala si mara mbili. 11 Basi mfalme wa Shamu moyo wake ukamfadhaika sana kwa ajili ya jambo hili; akawaita watumishi wake, akawaambia, Je! Hamtanionyesha, ni mtu yupi miongoni mwenu aliye upande wa mfalme wa Israeli? 12 Mmojawapo wa watumishi wake akasema, La, bwana wangu, mfalme; lakini Elisha, yule nabii aliye katika Israeli, humwambia mfalme wa Israeli maneno uyanenayo katika chumba chako cha kulala. 13 Akasema, Enendeni, mkamwangalie aliko, nipate kupeleka watu kwenda kumchukua. Akaambiwa ya kwamba, Tazama, yuko Dothani. 14 Kwa hiyo akapeleka huko farasi, na magari, na jeshi kubwa; wakafika usiku, wakauzingira mji ule pande zote. 15 Hata asubuhi na mapema mtumishi wake yule mtu wa Mungu alipoondoka, na kwenda nje, kumbe! Pana jeshi la watu, na farasi na magari, wameuzingira mji ule. Mtumishi wake akamwambia, Ole wetu! Bwana wangu, tufanyeje? 16 Akamjibu, Usiogope; maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao. 17 Elisha akaomba, akasema, Ee Bwana, nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona. Bwana akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona; na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote. 18 Na walipomtelemkia Elisha akamwomba Bwana, akasema, Uwapige, nakusihi, watu hawa kwa upofu. Akawapiga kwa upofu sawasawa na neno la Elisha. 19 Elisha akawaambia, Njia hii siyo, na mji huu sio, nifuateni mimi, nami nitawapeleka kwa mtu yule mnayemtafuta. Akawapeleka Samaria. 20 Hata walipokwisha kuingia Samaria, Elisha akasema, Bwana wafumbue macho watu hawa, wapate kuona. Bwana akawafumbua macho wakaona; kumbe! Walikuwa katikati ya Samaria. 21 Naye mfalme wa Israeli alipowaona, akamwambia Elisha, Ee baba yangu, niwapige? Niwapige? 22 Akamjibu, Usiwapige; je! Ungetaka kuwapiga watu ambao umewatwaa mateka kwa upanga wako na uta wako? Weka chakula na maji mbele yao, wapate kula na kunywa, na kwenda kwa bwana wao. 23 Basi akawaandalia chakula tele; nao walipokwisha kula na kunywa, akawaacha, wakaenda zao kwa bwana wao. Na vikosi vya Shamu havikuja tena katika nchi ya Israeli. 24 Ikawa baada ya hayo, Ben-hadadi mfalme wa Shamu akakusanya majeshi yake yote, akakwea akauhusuru Samaria. 25 Njaa ikawa kuu huko Samaria; na tazama, wakauhusuru, hata kichwa cha punda kikapata kuuzwa kwa vipande themanini vya fedha, na kibaba cha mavi ya njiwa kwa vipande vitano vya fedha. 26 Ikawa mfalme wa Israeli alipokuwa akipita ukutani, mwanamke mmoja akamwita akisema, Unisaidie, bwana wangu, mfalme. 27 Akasema, Bwana asipokusaidia, nikusaidieje mimi? Ya sakafuni, au ya shinikizoni? 28 Mfalme akamwambia, Una nini? Akajibu, Mwanamke huyu aliniambia, Mtoe mtoto wako, tumle leo, na mtoto wangu tutamla kesho. 29 Basi, tukamtokosa mtoto wangu, tukamla; nikamwambia siku ya pili, Mtoe mtoto wako, tumle; naye amemficha mtoto wake. 30 Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya huyo mwanamke, aliyararua mavazi yake; (naye alikuwa akipita juu ya ukuta;) na watu wakaona, na tazama, alikuwa amevaa magunia ndani mwilini mwake. 31 Ndipo akasema, Mungu anifanyie hivyo, na kuzidi, kikimbakia kichwa Elisha mwana wa Shafati juu yake leo. 32 Lakini Elisha alikuwa akikaa nyumbani mwake, na wazee wakikaa pamoja naye; na mfalme akamtuma mtu wa mbele yake; lakini hata kabla ya kufika kwake yule aliyetumwa, akawaambia wazee, Je! Mwaona jinsi huyu mwana wa mwuaji alivyotuma aniondolee kichwa changu? Angalieni, huyo aliyetumwa akifika, fungeni mlango, mkamzuie mlangoni; je! Sauti ya miguu ya bwana wake haiko nyuma yake? 33 Hata alipokuwa katika kusema nao, tazama, yule aliyetumwa akamshukia; naye akasema, Angalia, mabaya haya yatoka kwa Bwana; kwani mimi kumngojea Bwana tena?

2 Wafalme 7

1 Elisha akasema, Lisikieni neno la Bwana; Bwana asema hivi, Kesho panapo saa hii, kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, langoni pa Samaria. 2 Basi yule akida, ambaye mfalme alikuwa akitegemea mkono wake, akamjibu yule mtu wa Mungu, akasema, Tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akamwambia, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula. 3 Basi walikuwapo watu wanne wenye ukoma, penye lango la mji; wakasemezana, Mbona tunakaa hapa hata tufe? 4 Tukisema, Tutaingia mjini, mjini mna njaa, nasi tutakufa humo; nasi tukikaa hapa, tutakufa vile vile. Haya! Twende tukaliendee jeshi la Washami; wakituhifadhi hai tutaishi; wakituua, tutakufa tu. 5 Basi wakaondoka kabla ya mapambazuko, ili waende mpaka kituo cha Washami; na walipofika mwanzo wa kimo cha Washami, kumbe! Hapana mtu. 6 Kwa maana Bwana alikuwa amewasikizisha Washami kishindo cha miendo ya magari, na kishindo cha farasi, kama kishindo cha jeshi kubwa; wakaambiana, Tazama, mfalme wa Israeli amewaajiri wafalme wa Wahiti, na wafalme wa Wamisri, waje wapigane nasi. 7 Kwa hiyo wakaondoka, wakakimbia kungali giza bado, wakaziacha hema zao, na farasi zao, na punda zao, na kimo chao vile vile kama kilivyokuwa, wakakimbia wapate kujiponya nafsi zao. 8 Basi wale wenye ukoma walipofika mwisho wa kituo, waliingia katika hema moja, wakala, na kunywa, wakachukua fedha, na dhahabu, na mavazi, wakaenda wakavificha; wakarudi, wakaingia katika hema ya pili, vile vile wakachukua vitu, wakaenda, wakavificha. 9 Ndipo wakaambiana, Mambo haya tufanyayo si mema; leo ni siku ya habari njema, na sisi tunanyamaza; mkingoja hata kutakapopambazuka, madhara yatatupata; basi twende tukawaambie watu wa nyumba ya mfalme. 10 Basi wakaenda, wakawaita mabawabu wa mji; wakawaambia, Tulifika kituo cha Washami, na tazama, hapana mtu ye yote huko, wala sauti ya mtu, ila farasi wamefungwa, na punda wamefungwa, na hema zao kama walivyoziacha. 11 Na mabawabu wakaita wakawaambia watu wa nyumba ya mfalme. 12 Mfalme akaondoka usiku, akawaambia watumishi wake, Sasa nitawaonyesha ninyi walivyotutendea Washami. Wanajua ya kuwa tuna njaa; basi wametoka kituoni, ili kujificha kondeni, wakisema Watakapotoka mjini, tutawakamata hai; tena tutapata kuingia mjini. 13 Na mmojawapo wa watumishi wake akajibu, akasema, Kunradhi; baadhi ya watu na watwae farasi watano katika hao waliosalia, waliobaki ndani ya mji (tazama wamekuwa kama mkutano wote wa Israeli waliobaki ndani yake; tazama, wamekuwa kama mkutano wote wa Israeli walioangamia), tukawapeleke tukaone. 14 Basi wakatwaa magari mawili na farasi zake; mfalme akawatuma kuwafuata Washami, akasema, Enendeni, mkaangalie. 15 Wakawafuata mpaka Yordani; na kumbe! Njia yote ilikuwa imejaa mavazi na vyombo, walivyovitupa Washami, wapate kukimbia upesi. Watu wale waliotumwa wakarudi, wakamwambia mfalme. 16 Basi watu wakatoka, wakaziteka nyara hema za Washami. Ikawa kipimo cha unga mzuri kikauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, sawasawa na neno la Bwana. 17 Naye mfalme akamweka yule akida, ambaye alitegemea mkono wake, awasimamie watu langoni; na watu wakamkanyaga langoni, akafa; kama alivyosema yule mtu wa Mungu, aliyenena hapo mfalme alipomshukia. 18 Ikatukia kama vile yule mtu wa Mungu alivyomwambia mfalme, Vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, na kipimo cha unga mzuri kwa shekeli, ndivyo vitakavyokuwa kesho, panapo saa hii, katika lango la Samaria; 19 na yule akida akamjibu mtu wa Mungu, akasema, Sasa tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akasema, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula. 20 Ikampata vivyo hivyo, kwa kuwa watu wakamkanyaga langoni, akafa.

2 Wafalme 8

1 Basi Elisha alikuwa amemwambia yule mwanamke, ambaye alimfufulia mwanawe, akasema, Ondoka, ukaende wewe na jamaa yako, ukae hali ya kigeni utakakoweza kukaa; kwa sababu Bwana ameiita njaa; nayo itakuja juu ya nchi hii muda wa miaka saba. 2 Akaondoka yule mwanamke, akafanya kama alivyosema mtu wa Mungu; akaenda, yeye na jamaa yake, akakaa katika nchi ya Wafilisti miaka saba. 3 Ikawa miaka saba ilipoisha, yule mwanamke akarudi kutoka nchi ya Wafilisti; akatokea amlilie mfalme kwa ajili ya nyumba yake na shamba lake. 4 Basi mfalme alikuwa akizungumza na Gehazi, mtumishi wa mtu wa Mungu, akinena, Uniambie, nakusihi, mambo makuu yote aliyoyafanya Elisha. 5 Ikawa, alipokuwa katika kumwambia mfalme jinsi alivyomfufua mtu aliyekufa, tazama, huyo mwanamke aliyemfufulia mwanawe, alimlilia mfalme kwa ajili ya nyumba yake na shamba lake. Gehazi akasema, Bwana wangu mfalme, huyu ndiye mwanamke, na huyu ndiye mwanawe, ambaye Elisha alimfufua. 6 Na mfalme alipomwuliza yule mwanamke, yeye akamweleza. Basi mfalme akamtolea akida, akasema, Mrudishie yote aliyokuwa nayo, na mapato yote ya shamba lake tangu siku aliposafiri, hata leo. 7 Kisha, Elisha akaenda Dameski; na Ben-hadadi, mfalme wa Shamu, alikuwa hawezi; akaambiwa ya kwamba, Yule mtu wa Mungu amefika hapa. 8 Mfalme akamwambia Hazaeli, Chukua zawadi mkononi mwako, ukaende ili kumlaki yule mtu wa Mungu, ukamwulize Bwana kwa kinywa chake, kusema, Je! Nitapona ugonjwa huu? 9 Basi Hazaeli akaenda kumlaki, akachukua zawadi mkononi mwake, za kila kitu chema kilichopatikana Dameski, kiasi cha mizigo ya ngamia arobaini, akaenda, akasimama mbele yake akasema, Mwana wako Ben-hadadi, mfalme wa Shamu, amenituma kwako, kusema, Je nitapona ugonjwa huu? 10 Elisha akamwambia, Enenda, ukamwambie, Bila shaka utapona; lakini Bwana amenionyesha ya kwamba bila shaka atakufa. 11 Akamkazia macho hata akatahayari; na yule mtu wa Mungu akalia machozi. 12 Hazaeli akasema, Bwana wangu analilia nini? Akajibu, Kwa sababu nayajua mabaya utakayowatenda wana wa Israeli; utazichoma moto ngome zao, utawaua vijana wao kwa upanga, utawaseta-seta watoto wao wachanga na wanawake wao wenye mimba utawapasua. 13 Hazaeli akasema, Lakini mimi mtumwa wako ni nani, mimi niliye mbwa tu, hata nifanye jambo hili kubwa? Elisha akajibu, Bwana amenionyesha ya kwamba wewe utakuwa mfalme juu ya Shamu. 14 Ndipo akamwacha Elisha, akarudi kwa bwana wake; naye akamwambia, Elisha alikuambiaje? Akajibu, Aliniambia ya kuwa bila shaka utapona. 15 Ikawa siku ya pili yake, akatwaa tandiko la kitanda, akalichovya katika maji, akalitandaza juu ya uso wake, hata akafa. Na Hazaeli akatawala badala yake. 16 Katika mwaka wa tano wa Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, [Yehoshafati alipokuwa mfalme wa Yuda], alianza kutawala Yehoramu mwana wa Yehoshafati mfalme wa Yuda. 17 Alikuwa na umri wa miaka thelathini na miwili alipoanza kutawala, akatawala miaka minane huko Yerusalemu. 18 Akaiendea njia ya wafalme wa Israeli kama walivyofanya nyumba ya Ahabu; kwa kuwa alikuwa amemwoa binti Ahabu; akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana. 19 Walakini Bwana hakupenda kuiharibu Yuda, kwa ajili ya Daudi mtumishi wake, kama alivyomwahidia akasema, kuwa atampa taa, yeye na wazao wake siku zote. 20 Zamani zake, Edomu wakaasi mkononi mwa Yuda, wakajifanyia mfalme. 21 Basi akaenda Yehoramu mpaka Sairi, na magari yake yote pamoja naye. Akaondoka usiku, akawapiga Waedomi waliomzunguka yeye na maakida wa magari; na watu wakakimbilia hemani kwao. 22 Hivyo Edomu wakaasi mkononi mwa Yuda hata leo. Na Libna wakaasi zamani zizo hizo. 23 Na mambo yote ya Yehoramu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 24 Akalala Yehoramu na baba zake, akazikwa pamoja na baba zake mjini mwa Daudi; na Ahazia mwanawe akatawala mahali pake. 25 Katika mwaka wa kumi na mbili wa Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda alianza kutawala. 26 Ahazia alikuwa na umri wa miaka ishirini na miwili alipoanza kutawala; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu. Na jina la mamaye aliitwa Athalia binti Omri mfalme wa Israeli. 27 Akaiendea njia ya nyumba ya Ahabu, akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, kama walivyofanya nyumba ya Ahabu, kwa kuwa alikuwa mkwe wa jamaa ya Ahabu. 28 Akaenda pamoja na Yoramu mwana wa Ahabu ili kupigana na Hazaeli mfalme wa Shamu, huko Ramoth-gileadi; nao Washami wakamtia Yoramu jeraha. 29 Akarudi Yoramu mfalme, auguzwe katika Yezreeli jeraha walizotia Washami huko Rama alipopigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda akashuka amtazame Yoramu mwana wa Ahabu huko Yezreeli, kwa sababu alikuwa hawezi.

2 Wafalme 9

1 Nabii Elisha akamwita mmojawapo wa wana wa manabii, akamwambia, Jikaze viuno, ukachukue chupa hii ya mafuta mkononi mwako, ukaende Ramoth-Gileadi. 2 Utakapofika huko, mtafute Yehu, mwana wa Yehoshafati, mwana wa Nimshi, ukaingie, ukamtoe miongoni mwa ndugu zake, ukamchukue katika chumba cha ndani. 3 Kisha, ukatwae ile chupa ya mafuta, ukayamimine juu ya kichwa chake, ukaseme, Bwana asema hivi, Nimekutia mafuta uwe mfalme juu ya Israeli. Kisha ufungue mlango ukakimbie, wala usikawie. 4 Basi yule kijana, yule nabii kijana, akaenda Ramoth-Gileadi. 5 Naye alipofika, tazama, majemadari wa jeshi walikuwa wamekaa; naye akasema, Nimetumwa na neno kwako, Ee jemadari; Yehu akasema, Kwa yupi miongoni mwetu sote? Akasema, Kwako wewe, Ee jemadari. 6 Akainuka akaingia nyumbani; naye akayamimina yale mafuta kichwani mwake, akamwambia, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimekutia mafuta uwe mfalme juu ya watu wa Bwana, yaani, juu ya Israeli. 7 Nawe utawapiga nyumba ya Ahabu, bwana wako, ili nijilipize kisasi cha damu ya watumishi wangu manabii, na damu ya watumishi wote wa Bwana, mkononi mwa Yezebeli. 8 Kwa maana nyumba yote ya Ahabu wataangamia; nami nitamkatilia mbali kila mwanamume wa nyumba ya Ahabu, yeye aliyefungwa, na yeye asiyefungwa, katika Israeli. 9 Nami nitaifanya nyumba ya Ahabu kuwa kama nyumba ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na kama nyumba ya Baasha mwana wa Ahiya. 10 Na mbwa watamla Yezebeli katika kiwanja cha Yezreeli, wala hapatakuwa na mtu wa kumzika. Akaufungua mlango, akakimbia. 11 Ndipo Yehu akatoka akawaendea watumishi wa bwana wake. Mmoja wao akamwuliza, Je! Ni amani? Huyu mwenye wazimu amekujia kwa nini? Akawaambia, Ninyi mnamjua mtu huyu na habari ya maneno yake. 12 Wakasema, Ni uongo; haya, tuambie. Akasema, Aliniambia haya na haya, akisema, Bwana asema hivi, Nimekutia mafuta, uwe mfalme juu ya Israeli. 13 Basi wakafanya haraka, kila mtu akalitwaa vazi lake, na kulitia chini yake juu ya madaraja, wakapiga baragumu wakasema, Yehu ni mfalme. 14 Hivyo Yehu, mwana wa Yehoshafati, mwana wa Nimshi, akafanya fitina juu ya Yoramu. Basi Yoramu alikuwa akiulinda Ramoth-Gileadi, yeye na Israeli wote, kwa sababu ya Hazaeli mfalme wa Shamu. 15 Lakini mfalme Yoramu mwenyewe alikuwa amerudi, apate kupona jeraha zake alizotiwa na Washami, alipokuwa akipigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Yehu akasema, Kama hii ndiyo nia yenu, basi, msimwache hata mtu mmoja atoke mjini, ili aende kupeleka habari Yezreeli. 16 Basi Yehu akapanda gari lake kwenda Yezreeli; kwa maana Yoramu alikuwa amelala huko; na Ahazia mfalme wa Yuda alikuwa ameshuka ili kumtazama Yoramu. 17 Basi mlinzi alikuwa anasimama juu ya mnara wa Yezreeli, akaliona lile kundi la watu wa Yehu, alipokuwa akija, akasema, Naona kundi la watu. Yoramu akasema, Haya! Mtwae mpanda farasi mmoja, ukampeleke aende kuwalaki, na kuwauliza, Je! Ni amani? 18 Basi mpanda farasi mmoja akatoka awalaki, akasema, Mfalme asema hivi, Je! Ni amani? Yehu akasema, Wewe una nini na amani? Geuka unifuate. Yule mlinzi akatoa habari, akasema, Yule mjumbe amewafikilia, lakini harudi tena. 19 Ndipo akapeleka mpanda farasi wa pili, naye akawafikilia, akasema, Mfalme asema hivi, Je! Ni amani? Yehu akasema, Wewe una nini na amani? Geuka unifuate. 20 Yule mlinzi akatoa habari, akasema, Amewafikilia wala harudi tena; na mwendo huu ni kama mwendo wa Yehu mwana wa Nimshi; maana analiendesha gari kwa kasi. 21 Yoramu akasema, Tandika gari. Wakalitandika gari lake. Yoramu mfalme wa Israeli akatoka, na Ahazia mfalme wa Yuda, kila mtu katika gari lake. Wakatoka ili kumlaki Yehu, wakamkuta katika kiwanja cha Nabothi, Myezreeli. 22 Ikawa, Yoramu alipomwona Yehu, akasema, Je! Ni amani, Yehu? Akajibu, Amani gani, maadamu uzinzi wa mama yako Yezebeli na uchawi wake ni mwingi? 23 Yoramu akageuza mikono yake, akakimbia, akamwambia Ahazia, Ni uhaini, Ahazia. 24 Yehu akavuta upinde wake kwa nguvu zake zote, akampiga Yoramu kati ya mikono yake, hata mshale ukamtoka penye moyo wake, akaanguka katika gari lake. 25 Ndipo Yehu akamwambia Bidkari, akida wake, Mtwae ukamtupe katika kiwanja cha Nabothi, Myezreeli; maana kumbuka, hapo mimi na wewe tulipokuwa tumepanda farasi zetu, na kumfuata Anabu baba yake, Bwana alimwekea mzigo huu, akasema; 26 Hakika, jana nimeiona damu ya Nabothi, na damu ya wanawe, asema Bwana; nami nitakulipa katika kiwanja hiki, asema Bwana. Basi sasa mtwae huyu ukamtupe katika kiwanja hicho, sawasawa na neno la Bwana. 27 Na Ahazia mfalme wa Yuda alipoona hayo, akakimbia kwa njia ya nyumba ya bustanini. Yehu akamfuatia, akasema, Mpigeni huyu naye katika gari lake; wakampiga hapo penye kupandia Guri, karibu na Ibleamu. Akakimbilia Megido, akafa huko. 28 Na watumishi wake wakamchukua garini mpaka Yerusalemu, wakamzika katika kaburi lake pamoja na baba zake katika mji wa Daudi. 29 Katika mwaka wa kumi na moja wa Yoramu mwana wa Ahabu, Ahazia alianza kutawala juu ya Yuda. 30 Hata Yehu alipofika Yezreeli, Yezebeli akapata habari; akatia uwanja machoni mwake, akapamba kichwa chake, akachungulia dirishani. 31 Hata Yehu alipoingia lango la mji, alisema, Je! Ni amani, Ewe Zimri, mwenye kumwua bwana wako? 32 Akainua uso wake kulielekea dirisha, akasema, Aliye upande wangu ni nani? Matowashi wawili watatu wakachungulia. 33 Akasema, Mtupeni chini. Basi wakamtupa chini; na damu yake ikamwagika nyingine juu ya ukuta, na nyingine juu ya farasi, naye akamkanyaga-kanyaga. 34 Alipoingia, akala, na kunywa; kisha akasema, Haya! Mwangalieni mwanamke huyu aliyelaaniwa, mkamzike; kwa maana ni binti mfalme. 35 Wakaenda ili kumzika; lakini hawakuona kitu ila kifuvu cha kichwa chake, na miguu yake, na vitanga vya mikono yake. 36 Basi wakarudi, wakampasha habari. Akasema, Hili ndilo neno la Bwana, alilolinena kwa kinywa cha mtumishi wake Eliya, Mtishbi, kusema, Katika kiwanja cha Yezreeli mbwa wataila nyama ya Yezebeli. 37 Na mzoga wa Yezebeli utakuwa kama mavi juu ya uso wa mashamba, katika kiwanja cha Yezreeli; hata wasipate kusema, Huyu ni Yezebeli.

2 Wafalme 10

1 Basi Ahabu alikuwa na wana sabini katika Samaria. Yehu akaandika barua, akazipeleka Samaria kwa wakuu wa Yezreeli, yaani, wazee na hao walezi wa wana wa Ahabu, kusema, 2 Barua hii mara ikiwawasilia, kwa kuwa mna wana wa bwana wenu pamoja nanyi, tena kwenu kuna magari na farasi, na mji wenye boma, na silaha; 3 basi mtazameni yeye aliye mwema na hodari miongoni mwa wana wa bwana wenu, mkamweke kitini mwa babaye, mkaipiganie nyumba ya bwana wenu. 4 Lakini wao wakaogopa mno, wakasema, Tazama, wafalme wawili hawakusimama mbele yake; tupateje sisi kusimama? 5 Kisha yeye aliyekuwa juu ya nyumba, na yeye aliyekuwa juu ya mji, na wazee, na walezi, wakatuma ujumbe kwa Yehu, wakisema, Sisi tu watumwa wako, kila neno utakalotuambia, tutalifanya; hatutamfanya mtu awaye yote kuwa mfalme; ufanye yaliyo mema machoni pako. 6 Ndipo akawaandikia barua ya pili, kusema, Mkiwa upande wangu, na sauti yangu mkiisikia, vitwaeni vichwa vyao hao watu, wana wa bwana wenu, mkanijie kama wakati huu kesho hapa Yezreeli. Na hao wana wa mfalme, watu sabini, walikuwako kwa wakuu wa mji waliowalea. 7 Ikawa, barua ilipowawasilia, waliwatwaa hao wana wa mfalme, wakawaua, watu sabini, wakatia vichwa vyao katika makapu, wakampelekea huko Yezreeli. 8 Akaja mjumbe, akamwambia, akasema, Wamevileta vile vichwa vya wana wa mfalme. Akasema, Viwekeni chungu mbili penye maingilio ya lango hata asubuhi. 9 Ikawa asubuhi, akatoka, akasimama, akawaambia watu wote, Ninyi ni wenye haki; tazameni, mimi nalifanya fitina juu ya bwana wangu, nikamwua; ila ni nani aliyewapiga hawa wote? 10 Jueni basi ya kwamba halianguki chini lo lote la neno la Bwana, alilolinena Bwana juu ya nyumba ya Ahabu; kwa maana Bwana ameyafanya hayo aliyoyanena kwa kinywa cha mtumishi wake Eliya. 11 Hivyo Yehu akawapiga wote waliosalia wa nyumba ya Ahabu katika Yezreeli, na hao wakuu wake wote, na rafiki zake, na makuhani wake, hata hakumwachia aliyesalia hata mmoja. 12 Akaondoka, akashika njia akaenda Samaria. Hata njiani karibu na nyumba ya kukatia manyoya kondoo, ya wachungaji. 13 Yehu akakutana na ndugu za Ahazia mfalme wa Yuda, akawauliza, Ni nani ninyi? Wakamjibu, Sisi tu ndugu zake Ahazia; tunashuka kuwasalimu wana wa mfalme na wana wa malkia. 14 Akasema, Wakamateni wa hai. Wakawakamata wa hai, wakawaua penye birika ya nyumba ya kukatia manyoya kondoo, watu arobaini na wawili; wala hakumsaza mtu wao awaye yote. 15 Alipotoka huko akamkuta Yehonadabu mwana wa Rekabu akija kumlaki; akamsalimu akamwambia, Je! Moyo wako umenyoka, kama moyo wangu ulivyo pamoja na moyo wako? Akajibu Yehonadabu, Ndio. Yehu akamwambia, Kama ndio, nipe mkono wako. Akampa mkono, akamkalisha pamoja naye garini. 16 Akasema, Fuatana nami, ukaone wivu wangu kwa Bwana. Wakampandisha garini mwake. 17 Naye alipofika Samaria, aliwapiga wote waliomsalia Ahabu katika Samaria, hata akamwangamiza, sawasawa na neno la Bwana alilomwambia Eliya. 18 Yehu akawakusanya watu wote, akawaambia, Ahabu alimtumikia Baali kidogo; bali Yehu atamtumikia sana. 19 Basi niitieni manabii wote wa Baali, wote wamwabuduo, na makuhani wake wote; mtu asikose kuwapo hata mmoja. Maana ninayo dhabihu kubwa ya kumtolea Baali; ye yote atakayekosa kuwapo hataishi. Lakini Yehu alifanya hayo kwa hila, ili awaharibu waliomwabudu Baali. 20 Yehu akasema, Takaseni kusanyiko la dini kwa Baali. Wakalitangaza. 21 Yehu akatuma wajumbe katika Israeli yote, nao wote waliomwabudu Baali wakaja, wala hakusalia mtu ye yote asiyekuja. Wakaingia nyumbani mwa Baali; ikajaa nyumba ya Baali tangu mlango hata mlango. 22 Akamwambia yule aliyekuwa juu ya hazina ya mavazi, Uwatolee mavazi wote wanaomwabudu Baali. Akawatolea mavazi. 23 Akaingia Yehu na Yehonadabu mwana wa Rekabu nyumbani mwa Baali, akawaambia waliomwabudu Baali, Tafuteni mkaangalie, asiwepo hapa pamoja nanyi mtu amtumikiaye Bwana, ila wamwabuduo Baali peke yao. 24 Wakaingia ili watoe dhabihu na sadaka za kuteketezwa. Basi Yehu alikuwa amejiwekea nje watu themanini, akasema, Mtu mmoja akiokoka wa watu niliowatia mikononi mwenu, amwachaye huyo, roho yake itakuwa badala ya roho yake. 25 Ikawa mara alipokwisha kutoa sadaka ya kuteketezwa, Yehu akawaambia walinzi na maakida, Ingieni mwapige; mtu awaye yote asitoke. Basi wakawapiga kwa makali ya upanga; walinzi na maakida wakawatupa nje, wakaenda mpaka mji wa nyumba ya Baali. 26 Wakazitoa nguzo zilizokuwamo nyumbani mwa Baali, wakaziteketeza. 27 Wakaibomoa nguzo ya Baali, na kuiangusha nyumba ya Baali, wakaifanya choo hata leo. 28 Ndivyo Yehu alivyomharibu Baali katika Israeli. 29 Walakini katika makosa yake Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli, Yehu hakutoka katika kuyafuata, yaani, ndama za dhahabu zilizokuwako katika Betheli na Dani. 30 Bwana akamwambia Yehu, Kwa kuwa umetenda vema kwa kufanya vilivyo haki machoni pangu, kuitendea nyumba ya Ahabu sawasawa na yote yaliyomo moyoni mwangu, wana wako wa kizazi cha nne watakaa kitini mwa Israeli. 31 Lakini Yehu hakuangalia, aende katika sheria ya Bwana, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote; hakutoka katika makosa ya Yeroboamu, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli. 32 Siku zile Bwana akaanza kupunguza Israeli. Hazaeli akawapiga mipakani mwote mwa Israeli; 33 kutoka Yordani upande wa mashariki, nchi yote ya Gileadi, na ya Wagadi, na Wareubeni, na Wamanase, kutoka Aroeri iliopo karibu na bonde la Arnoni, yaani, Gileadi, na Bashani. 34 Basi mambo yote ya Yehu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, na ushujaa wake, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 35 Yehu akalala na babaze; wakamzika katika Samaria. Na Yehoahazi mwanawe akatawala mahali pake. 36 Na muda Yehu aliotawala juu ya Israeli katika Samaria ulikuwa miaka ishirini na minane.

2 Wafalme 11

1 Na Athalia, mama yake Ahazia, alipoona ya kuwa mwanawe amekufa, akainuka, akawaharibu wazao wote wa kifalme. 2 Ila Yehosheba, binti wa mfalme Yehoramu, umbu lake Ahazia ,akamtwaa Yoashi mwana wa Ahazia ,akamwiba miongoni mwa hao wana wa mfalme waliouawa ,yeye na mlezi wake ,na kuwatia katika chumba cha kulala;wakamficha usoni pa Athalia,basi kwa hiyo hakuuawa. 3 Alikuwako pamoja naye, amefichwa nyumbani mwa Bwana, miaka sita. Naye Athalia akaitawala nchi. 4 Hata mwaka wa saba Yehoyada akatuma, na kuwaleta wakuu wa mamia, wa Wakari, na wa walinzi, akawaleta kwake ndani ya nyumba ya Bwana; akapatana nao, akawaapisha nyumbani mwa Bwana, akawaonyesha huyo mwana wa mfalme. 5 Akawaamuru, akasema, Hili ndilo neno mtakalolifanya; theluthi yenu, mtakaoingia siku ya sabato, mtayalinda malinzi ya nyumba ya mfalme; 6 na theluthi mtakuwapo mlangoni pa Suri; na theluthi langoni nyuma ya walinzi; hivyo mtayalinda malinzi ya nyumba, kuzuia watu wasiingie. 7 Na sehemu mbili zenu, yaani, wote watokao siku ya sabato, mtayalinda malinzi ya nyumba ya Bwana kumzunguka mfalme. 8 Mtamzunguka mfalme pande zote, kila mtu mwenye silaha zake mkononi; naye awaye yote aingiaye ndani ya safu auawe; mkafuatane na mfalme, akitoka na akiingia. 9 Nao wakuu wa mamia wakafanya sawasawa na yote aliyowaamuru Yehoyada kuhani; wakawatwaa kila mtu watu wake, hao watakaoingia sabato, nao watakaotoka sabato, wakaja kwa Yehoyada kuhani. 10 Naye yule kuhani akawapa wakuu wa mamia mikuki na ngao zilizokuwa za mfalme Daudi, zilizokuwamo nyumbani mwa Bwana. 11 Walinzi wakasimama, kila mtu na silaha zake mkononi, kutoka pembe ya kuume ya nyumba mpaka pembe ya kushoto ya nyumba, kando ya madhabahu na nyumba, wakimzunguka mfalme pande zote. 12 Ndipo akamleta nje mwana wa mfalme, akamvika taji, na kumpa ushuhuda; wakamfanya mfalme, wakamtia mafuta; wakapiga makofi, wakasema, mfalme na aishi. 13 Na Athalia alipoisikia sauti ya walinzi na ya watu, aliingia kwa watu nyumbani kwa Bwana; 14 akatazama, na tazama, mfalme amesimama karibu na nguzo kama ilivyokuwa desturi, nao wakuu na wapiga baragumu karibu na mfalme; na watu wote wa nchi wakafurahi, wakapiga baragumu. Ndipo Athalia akararua mavazi yake, akalia, Fitina! Fitina! 15 Naye Yehoyada kuhani akawaamuru wakuu wa mamia, majemadari wa jeshi, akawaambia, Mtoeni kati ya safu; naye ye yote amfuataye mwueni kwa upanga. Kwani kuhani akasema, Asiuawe nyumbani mwa Bwana. 16 Basi wakampisha njia; akaenda kwa njia ya kuingia kwa farasi nyumbani mwa mfalme; akauawa huko. 17 Kisha, Yehoyada akafanya mapatano kati ya Bwana na mfalme na watu, ili wawe watu wa Bwana; tena kati ya mfalme na watu. 18 Watu wote wa nchi wakaiendea nyumba ya Baali, wakaiangusha; madhabahu zake na sanamu zake wakazivunja-vunja kabisa, na Matani kuhani wa Baali wakamwua mbele ya madhabahu. Na Yehoyada kuhani akaweka maakida juu ya nyumba ya Bwana. 19 Akawatwaa wakuu wa mamia, na Wakari, na walinzi, na watu wote wa nchi; wakamleta mfalme kushuka nyumbani mwa Bwana, wakaja kwa njia ya mlango wa walinzi mpaka nyumba ya mfalme. Naye akakaa katika kiti cha enzi cha wafalme. 20 Basi watu wote wa nchi wakafurahi, na mji ukatulia. Naye Athalia wakamwua kwa upanga karibu na nyumba ya mfalme. 21 Yoashi alikuwa na umri wa miaka saba alipoanza kutawala.

2 Wafalme 12

1 Katika mwaka wa saba wa Yehu, Yoashi alianza kutawala; akatawala miaka arobaini huko Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Sibia wa Beer-sheba. 2 Yoashi akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana siku zake zote Yehoyada kuhani alizomfundisha. 3 Ila mahali pa juu hapakuondolewa; watu wakaendelea kutoa sadaka na kufukiza uvumba katika mahali pa juu. 4 Yoashi akawaambia makuhani, Fedha yote ya vitu vitakatifu iliyoletwa nyumbani mwa Bwana, fedha ya matumizi, fedha ya watu kadiri alivyoandikiwa kila mtu, na fedha yote iliyoletwa kama mtu ye yote aonavyo moyoni mwake kuileta nyumbani mwa Bwana, 5 makuhani na waitwae, kila mtu kwa hao awajuao; nao watatengeneza palipobomoka nyumbani, kila mahali palipoonekana pamebomoka. 6 Lakini ikawa, mwaka wa ishirini na tatu wa mfalme Yoashi, makuhani walikuwa hawajatengeneza mabomoko ya nyumba. 7 Ndipo mfalme Yoashi akamwita Yehoyada kuhani, na makuhani wengine, akawauliza, Mbona hamtengenezi mabomoko ya nyumba? Basi sasa msipokee tena fedha kwa hao mwajuao, lakini itoeni kwa ajili ya mabomoko ya nyumba. 8 Nao makuhani wakakubali kwamba wasipokee fedha kwa watu, wala wasitengeneze mabomoko ya nyumba. 9 Lakini Yehoyada kuhani akatwaa kasha, akatoboa tundu katika kifuniko chake, akaliweka karibu na madhabahu, upande wa kuume mtu aingiapo nyumbani mwa Bwana; na makuhani, waliolinda mlangoni, wakatia ndani yake fedha yote iliyoletwa nyumbani mwa Bwana. 10 Ikawa, walipoona ya kuwa fedha nyingi imo kashani, karani wa mfalme akapanda na kuhani mkuu, wakaifunga mifukoni, wakaihesabu fedha iliyoonekana nyumbani mwa Bwana. 11 Na fedha iliyopimwa wakawapa mikononi wale waliofanya kazi, walioisimamia nyumba ya Bwana; na hao wakawatolea maseremala na wajenzi walioifanya kazi katika nyumba ya Bwana, 12 na hao waashi, na wakata mawe, tena kununua miti na mawe ya kuchongwa, ili kuyatengeneza mabomoko ya nyumba ya Bwana, tena kwa gharama zote za kuitengeneza nyumba. 13 Lakini havikufanywa kwa nyumba ya Bwana vikombe vya fedha, wala makasi, wala mabakuli, wala panda, wala vyombo vyo vyote vya dhahabu, wala vyombo vya fedha, kwa hiyo fedha iliyoletwa nyumbani mwa Bwana; 14 kwa sababu hiyo fedha waliwapa watenda kazi, wakaitengeneza kwayo nyumba ya Bwana. 15 Walakini hawakufanya hesabu na hao watu, waliokabidhiwa fedha hiyo ili wawape watenda kazi; kwa kuwa walitenda kwa uaminifu. 16 Lakini fedha ya matoleo ya kosa, na fedha ya matoleo ya dhambi, haikuletwa nyumbani mwa Bwana; hiyo ilikuwa ya makuhani wenyewe. 17 Ndipo akakwea Hazaeli mfalme wa Shamu akapigana na Gathi, akautwaa; Hazaeli akaelekeza uso ili akwee kwenda Yerusalemu. 18 Yoashi mfalme wa Yuda akavitwaa vyote alivyoviweka wakfu Yehoshafati, na Yehoramu, na Ahazia, baba zake, wafalme wa Yuda, navyo vyote alivyoweka wakfu mwenyewe, na dhahabu yote iliyoonekana katika hazina za nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme, akamletea Hazaeli mfalme wa Shamu; basi akaenda zake kutoka Yerusalemu. 19 Basi mambo yote ya Yoashi yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 20 Nao watumishi wake wakaondoka, wakafanya fitina, wakamwua Yoashi katika nyumba ya Milo, hapo panaposhukia Sila. 21 Kwa maana Yozakari mwana wa Shimeathi, na Yehozabadi mwana wa Shomeri, watumishi wake, wakampiga, naye akafa; wakamzika pamoja na babaze mjini mwa Daudi. Na Amazia mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 13

1 Katika mwaka wa ishirini na tatu wa Yoashi mwana wa Ahazia, mfalme wa Yuda, Yehoahazi mwana wa Yehu alianza kutawala juu ya Israeli katika Samaria; akatawala miaka kumi na saba. 2 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, akayafuata makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli; wala hakuyaacha. 3 Hasira ya Bwana ikawaka juu ya Israeli, akawatia mkononi mwa Hazaeli mfalme wa Shamu, na mkononi mwa Ben-hadadi mwana wa Hazaeli, siku zote. 4 Naye Yehoahazi akamsihi Bwana, Bwana akamsikiliza; kwa kuwa aliyaona mateso ya Israeli, jinsi mfalme wa Shamu alivyowatesa. 5 (Bwana akawapa Israeli mwokozi, nao wakatoka mikononi mwa Washami; wana wa Israeli wakakaa hemani mwao kama zamani za kwanza. 6 Lakini hawakuyaacha makosa ya nyumba ya Yeroboamu, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli, lakini wakaendelea katika hayo; nayo ile Ashera ikakaa vivyo katika Samaria). 7 Kwa kuwa hakumwachia Yehoahazi watu ila wapandao farasi hamsini, na magari kumi, na askari elfu kumi waendao kwa miguu; kwa kuwa mfalme wa Shamu aliwaharibu, akawaponda mfano wa mavumbi yaliyokanyagwa. 8 Basi mambo yote ya Yehoahazi yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, na ushujaa wake, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 9 Yehoahazi akalala na babaze; wakamzika katika Samaria. Na Yehoashi mwanawe akatawala mahali pake. 10 Katika mwaka wa thelathini na saba wa Yoashi mfalme wa Yuda, Yehoashi mwana wa Yehoahazi alianza kutawala juu ya Israeli katika Samaria, akatawala miaka kumi na sita. 11 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana; hakuyaacha makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli; lakini akaendelea katika hayo. 12 Basi mambo yote ya Yehoashi yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, na ushujaa wake aliopigania na Amazia mfalme wa Yuda, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 13 Yehoashi akalala na babaze; na Yeroboamu akakaa katika kiti chake cha enzi; naye Yehoashi akazikwa huko Samaria, pamoja na wafalme wa Israeli. 14 Basi Elisha alikuwa ameshikwa na ugonjwa wake uliomwua; naye Yehoashi mfalme wa Israeli akatelemka amtazame, akamlilia mbele yake, akasema, Baba yangu! Baba yangu! Gari la Israeli na wapanda farasi wake! 15 Elisha akamwambia, Twaa uta na mishale; naye akatwaa uta na mishale. 16 Akamwambia mfalme wa Israeli, Weka mkono wako katika uta; naye akaweka mkono wake juu yake. Elisha akaweka mikono yake juu ya mikono ya mfalme. 17 Akasema, Lifungue dirisha linaloelekea mashariki; akalifungua. Basi Elisha akasema, Piga; akapiga. Akasema, Mshale wa Bwana wa kushinda, naam, mshale wa kushinda Shamu, kwa maana utawapiga Washami katika Afeki hata utakapowaangamiza. 18 Akasema, Itwae mishale; akaitwaa. Akamwambia mfalme wa Israeli, Piga chini; akaipiga nchi mara tatu, akaacha. 19 Yule mtu wa Mungu akamkasirikia, akasema, Ingalikupasa kupiga mara tano au mara sita; ndipo ungaliipiga Shamu hata kuiangamiza; bali sasa utaipiga Shamu mara tatu tu. 20 Elisha akafa, nao wakamzika. Basi vikosi vya Wamoabi wakaingia katika nchi mwanzo wa mwaka. 21 Ikawa, walipokuwa wakimzika mtu, angalia, waliona kikosi; wakamtupa yule mtu kaburini mwa Elisha; mara yule maiti alipoigusa mifupa ya Elisha, alifufuka, akasimama kwa miguu. 22 Na Hazaeli mfalme wa Shamu akawaonea Israeli siku zote za Yehoahazi. 23 Lakini Bwana akawahurumia, akawasikitikia, na kuwaangalia, kwa ajili ya agano lake na Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, wala hakutaka kuwaangamiza, wala hakuwatupa usoni pake bado. 24 Akafa Hazaeli mfalme wa Shamu, na Ben-hadadi mwanawe akatawala mahali pake. 25 Naye Yehoashi, mwana wa Yehoahazi, akaitwaa tena mkononi mwa Ben-hadadi mwana wa Hazaeli miji ile aliyoitwaa yeye mkononi mwa Yehoahazi baba yake vitani. Mara tatu Yehoashi akamshinda, akairudisha miji ya Israeli.

2 Wafalme 14

1 Katika mwaka wa pili wa Yehoashi mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli Amazia mwana wa Yoashi mfalme wa Yuda alianza kutawala. 2 Naye alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka ishirini na kenda katika Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Yehoadani wa Yerusalemu. 3 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, ila si kama babaye Daudi; akafanya kama yote aliyoyafanya baba yake Yoashi. 4 Walakini mahali pa juu hapakuondolewa; watu wakaendelea kutoa dhabihu na kufukiza uvumba katika mahali pa juu. 5 Ikawa, mara ufalme ulipokuwa imara mkononi mwake, aliwaua watumishi wale waliomwua mfalme baba yake; 6 ila hakuwaua watoto wa hao wauaji; kama ilivyoandikwa katika kitabu cha torati ya Musa, kama alivyoamuru Bwana, akisema, Mababa wasife kwa makosa ya wana, wala wana wasife kwa makosa ya mababa; lakini kila mtu atakufa kwa kosa lake mwenyewe. 7 Akawaua Waedomi katika Bonde la Chumvi watu elfu kumi; akautwaa Sela vitani, akauita jina lake Yoktheeli hata leo. 8 Ndipo Amazia akatuma wajumbe kwa Yehoashi mwana wa Yehoahazi mwana wa Yehu, mfalme wa Israeli, akisema, Njoo, tutazamane uso kwa uso. 9 Naye Yehoashi mfalme wa Israeli akatuma kwa Amazia mfalme wa Yuda, akisema, Mbaruti uliokuwako Lebanoni ulituma kwa mwerezi uliokuwako Lebanoni, kusema, Umwoze mwanangu binti yako; kukapita hayawani aliyekuwako Lebanoni, akaukanyaga ule mbaruti. 10 Kweli umepiga Edomu, na moyo wako umekutukuza; ujisifu basi, ukae nyumbani mwako. Mbona unataka kujitia bure katika madhara, hata uanguke, wewe na Yuda pamoja nawe? 11 Lakini Amazia hakutaka kusikia. Basi Yehoashi mfalme wa Israeli akakwea; wakatazamana uso kwa uso, yeye na Amazia mfalme wa Yuda, huko Beth-shemeshi ulio wa Yuda. 12 Yuda wakashindwa mbele ya Israeli; wakakimbia kila mtu hemani kwake. 13 Yehoashi mfalme wa Israeli akamtwaa Amazia mfalme wa Yuda, mwanawe Yoashi mwana wa Ahazia, huko Beth-shemeshi, akaja Yerusalemu, akauvunja ukuta wa Yerusalemu toka lango la Efraimu hata lango la pembeni, mikono mia nne. 14 Akaitwaa dhahabu yote na fedha, na vyombo vyote vilivyoonekana katika nyumba ya Bwana, na katika hazina za nyumba ya mfalme, tena watu, kuwa amana; akarudi Samaria. 15 Basi mambo yote ya Yehoashi yaliyosalia, aliyoyafanya, na ushujaa wake, na jinsi alivyopigana na Amazia mfalme wa Yuda, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 16 Yehoashi akalala na baba zake, akazikwa katika Samaria pamoja na wafalme wa Israeli; na Yeroboamu mwanawe akatawala mahali pake. 17 Naye Amazia mwana wa Yoashi mfalme wa Yuda akaishi baada ya kufa kwake Yehoashi mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli miaka kumi na mitano. 18 Basi mambo yote ya Amazia yaliyosalia, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 19 Wakafanya fitina juu yake katika Yerusalemu, naye akakimbia mpaka Lakishi, lakini wakatuma watu kumfuata mpaka Lakishi, wakamwua huko. 20 Wakamleta juu ya farasi; naye akazikwa huko Yerusalemu pamoja na babaze katika mji wa Daudi. 21 Na watu wote wa Yuda wakamtwaa Uzia aliyekuwa mwenye umri wa miaka kumi na sita,wakamfanya awe mfalme mahali pa baba yake Amazia. 22 Huyo akajenga Elathi, akaurudisha kwa Yuda, baada ya kulala mfalme pamoja na babaze. 23 Katika mwaka wa kumi na tano wa Amazia mwana wa Yoashi mfalme wa Yuda Yeroboamu mwana wa Yehoashi mfalme wa Israeli alianza kutawala katika Samaria; akatawala miaka arobaini na mmoja. 24 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana; wala hakuyaacha makosa yote ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli. 25 Yeye akaurudisha mpaka wa Israeli toka kuingia kwa Hamathi hata bahari ya Araba, sawasawa na neno la Bwana, Mungu wa Israeli, alilolinena kwa mkono wa mtumishi wake Yona mwana wa Amitai, nabii, aliyekuwa wa Gath-heferi. 26 Kwani Bwana akayaona mateso ya Israeli, kwamba yalikuwa machungu sana; maana hakukuwa na mfungwa wala asiyefungwa, wala msaidizi kwa ajili ya Israeli. 27 Wala Bwana hakusema ya kwamba atalifuta jina la Israeli litoke chini ya mbingu; lakini akawaokoa kwa mkono wa Yeroboamu mwana wa Yehoashi. 28 Basi mambo yote ya Yeroboamu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, na ushujaa wake, na jinsi aliyvopigana, akawapatia tena Israeli Dameski na Hamathi, iliyokuwa kwanza ya Yuda, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 29 Yeroboamu akalala na babaze, yaani, na wafalme wa Israeli. Na Zekaria mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 15

1 Katika mwaka wa ishirini na saba wa Yeroboamu mfalme wa Israeli Uzia mwana wa Amazia mfalme wa Yuda alianza kutawala. 2 Alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala; akatawala miaka hamsini na miwili huko Yerusalemu. Na jina la mamaye aliitwa Yekolia wa Yerusalemu. 3 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, kama yote aliyoyafanya babaye Amazia. 4 Ila mahali pa juu hapakuondolewa, nao watu wakaendelea kutoa sadaka na kufukiza uvumba katika mahali pa juu. 5 Bwana akampiga mfalme, akawa na ukoma hata siku ya kufa kwake, akakaa katika nyumba ya pekee. Na Yothamu mwana wa mfalme alikuwa juu ya nyumba, akiwahukumu watu wa nchi. 6 Basi mambo yote ya Uzia yaliyosalia, nayo yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 7 Uzia akalala na babaze; wakamzika pamoja na babaze mjini mwa Daudi; na Yothamu mwanawe akatawala mahali pake. 8 Katika mwaka wa thelathini na nane wa Uzia mfalme wa Yuda Zekaria mwana wa Yeroboamu akatawala juu ya Israeli katika Samaria miezi sita. 9 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana kama walivyofanya babaze; hakuyaacha makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli. 10 Na Shalumu mwana wa Yabeshi akafanya fitina juu yake, akampiga mbele ya watu, akamwua, akatawala mahali pake. 11 Basi mambo yote ya Zekaria yaliyosalia, tazama, yameandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli. 12 Hilo ndilo neno la Bwana alilomwambia Yehu, akisema, Wana wako watakaa kitini mwa Israeli hata kizazi cha nne. Ikawa vivyo hivyo. 13 Huyo Shalumu mwana wa Yabeshi alianza kutawala katika mwaka wa thelathini na kenda wa Uzia mfalme wa Yuda; akatawala muda wa mwezi mmoja katika Samaria. 14 Menahemu mwana wa Gadi akapanda kutoka Tirza, akaja Samaria, akampiga Shalumu mwana wa Yabeshi huko Samaria, akamwua, akatawala mahali pake. 15 Basi mambo yote ya Shalumu yaliyosalia, na fitina aliyoifanya, tazama, yameandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli. 16 Ndipo Menahemu akapiga Tifsa, na wote waliokuwamo, na mipaka yake, toka Tirza; kwa sababu hawakumfungulia, kwa hiyo akaupiga; nao wanawake wote waliokuwamo wenye mimba akawapasua. 17 Katika mwaka wa thelathini na kenda wa Uzia mfalme wa Yuda Menahemu mwana wa Gadi alianza kutawala juu ya Israeli, akatawala miaka kumi katika Samaria. 18 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana; hakuyaacha siku zake zote makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli. 19 Akaja Pulu mfalme wa Ashuru juu ya nchi; naye Menahemu akampa Pulu talanta elfu za fedha, ili kwamba mkono wake uwe pamoja naye, na ufalme uwe imara mkononi mwake. 20 Na Menahemu akawatoza Israeli fedha hiyo, yaani, wakuu wote wenye mali, kila mtu shekeli hamsini za fedha, ili ampe huyo mfalme wa Ashuru. Basi mfalme wa Ashuru akarejea, wala hakukaa huko katika nchi. 21 Basi mambo yote ya Menahemu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli? 22 Menahemu akalala na babaze; na Pekahia mwanawe akatawala mahali pake. 23 Katika mwaka wa hamsini wa Uzia mfalme wa Yuda Pekahia mwana wa Menahemu alianza kutawala juu ya Israeli hatika Samaria; akatawala miaka miwili. 24 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana; hakuyaacha makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli. 25 Na Peka mwana wa Remalia, jemadari wake, akamfanyia fitina, akampiga huko Samaria, katika ngome ya nyumba ya mfalme, pamoja na Argobu na Arie; na pamoja naye walikuwako watu hamsini wa Wagileadi. Akamwua, akatawala mahali pake. 26 Basi mambo yote ya Pekahia yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, tazama, yameandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli. 27 Katika mwaka wa hamsini na mbili wa Uzia mfalme wa Yuda Peka mwana wa Remalia alianza kutawala juu ya Israeli katika Samaria; akatawala miaka ishirini. 28 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana; hakuyaacha makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambayo kwa hayo aliwakosesha Israeli. 29 Katika siku za Peka mfalme wa Israeli akaja Tiglath-pileseri mfalme wa Ashuru, akatwaa Iyoni, na Abel-beth-maaka, na Yanoa, na Kedeshi, na Hazori, na Gileadi, na Galilaya, nchi yote ya Naftali; akawahamisha hao watu mpaka Ashuru. 30 Na Hoshea mwana wa Ela akafanya fitina juu ya Peka mwana wa Remalia, akampiga, akamwua, akatawala mahali pake, katika mwaka wa ishirini wa Yothamu mwana wa Uzia. 31 Basi mambo yote ya Peka yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, tazama, yameandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Israeli. 32 Katika mwaka wa pili wa Peka mwana wa Remalia mfalme wa Israeli Yothamu mwana wa Uzia mfalme wa Yuda alianza kutawala. 33 Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka kumi na sita katika Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Yerusha binti Sadoki. 34 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana; akafanya kama yote aliyoyafanya Uzia baba yake. 35 Ila mahali pa juu hapakuondolewa; watu walikuwa wakitoa sadaka na kufukiza uvumba katika mahali pa juu. Ndiye aliyelijenga lango la juu la nyumba ya Bwana. 36 Basi mambo yote ya Yothamu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 37 Zamani hizo akaanza Bwana kumtuma juu ya Yuda Resini mfalme wa Shamu, na Peka mwana wa Remalia. 38 Yothamu akalala na babaze, akazikwa pamoja na babaze katika mji wa Daudi baba yake. Na Ahazi mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 16

1 Katika mwaka wa kumi na saba wa Peka mwana wa Remalia Ahazi mwana wa Yothamu mfalme wa Yuda alianza kutawala. 2 Alikuwa na umri wa miaka ishirini alipoanza kutawala; akatawala miaka kumi na sita katika Yerusalemu; wala hakufanya mema machoni pa Bwana Mungu wake, kama Daudi babaye. 3 Lakini aliiendea njia ya wafalme wa Israeli, hata akampitisha mwanawe motoni, sawasawa na machukizo ya mataifa Bwana aliowafukuza mbele ya wana wa Israeli. 4 Kisha akatoa sadaka na kufukiza uvumba katika mahali pa juu, na juu ya vilima, na chini ya kila mti mbichi. 5 Hapo ndipo akakwea Resini mfalme wa Shamu pamoja na Peka mwana wa Remalia mfalme wa Israeli juu ya Yerusalemu ili wapigane; wakamhusuru Ahazi, ila hawakuweza kumshinda. 6 Wakati huo Resini mfalme wa Shamu akawarudishia Washami Elathi, akawafukuza Wayahudi kutoka Elathi; nao Washami wakaja Elathi, wakakaa humo hata leo. 7 Basi Ahazi akatuma wajumbe kwa Tiglath-pileseri mfalme wa Ashuru, akasema, Mimi ni mtumishi, tena mwana wako; kwea, ukaniokoe mkononi mwa mfalme wa Shamu, na mkononi mwa mfalme wa Israeli, walioniinukia. 8 Ahazi akatwaa fedha na dhahabu iliyoonekana katika nyumba ya Bwana, na katika hazina za nyumba ya mfalme, akazipeleka kwa mfalme wa Ashuru kuwa zawadi. 9 Na huyo mfalme wa Ashuru akamsikia; mfalme wa Ashuru akapanda juu ya Dameski, akautwaa, akawahamisha watu wake mateka mpaka Kiri, akamwua Resini. 10 Naye mfalme Ahazi akaenda Dameski ili aonane na Tiglath-pileseri mfalme wa Ashuru, akaiona ile madhabahu iliyokuwako Dameski. Mfalme Ahazi akamletea Uria kuhani namna yake ile madhabahu, na cheo chake, kama ilivyokuwa kazi yake yote. 11 Naye Uria kuhani akajenga madhabahu; sawasawa na yote aliyomletea mfalme Ahazi kutoka Dameski; ndivyo alivyoifanya Uria kuhani iwe tayari atakaporudi mfalme Ahazi kutoka Dameski. 12 Na mfalme aliporudi kutoka Dameski, mfalme akaiona ile madhabahu; mfalme akakaribia madhabahuni, na kutoa sadaka juu yake. 13 Akaiteketeza sadaka yake ya kuteketezwa, na sadaka yake ya unga, akamimina sadaka yake ya kinywaji, akanyunyiza damu ya sadaka zake za amani, juu ya madhabahu. 14 Na ile madhabahu ya shaba iliyokuwako mbele za Bwana, akaileta kutoka mbele ya nyumba, kutoka kati ya madhabahu yake mwenyewe na nyumba ya Bwana, akaiweka upande wa kaskazini wa madhabahu yake. 15 Mfalme Ahazi akamwamuru Uria kuhani, akisema, Juu ya madhabahu hiyo kubwa uiteketeze sadaka ya kuteketezwa ya asubuhi, na sadaka ya unga ya jioni, na sadaka ya mfalme ya kuteketezwa, na sadaka yake ya unga, pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya watu wote wa nchi, na sadaka yao ya unga, na sadaka zao za kinywaji; ukanyunyize juu yake damu yote ya sadaka ya kuteketezwa, na damu yote ya dhabihu; bali madhabahu ya shaba itakuwa kwangu mimi ili niiulizie. 16 Akafanya hivyo Uria kuhani, sawasawa na yote aliyoyaamuru mfalme Ahazi. 17 Mfalme Ahazi akakata papi za matako, akaliondoa lile birika juu yake; akaitelemsha ile bahari itoke juu ya ng'ombe za shaba zilizokuwa chini yake, akaiweka juu ya sakafu ya mawe. 18 Na ukumbi wa sabato walioujenga katika hiyo nyumba, na mahali pa kuingia pake mfalme palipokuwapo nje, akavigeuza kuikabili nyumba ya Bwana, kwa sababu ya mfalme wa Ashuru. 19 Basi mambo yote ya Ahazi yaliyosalia, aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 20 Ahazi akalala na babaze, akazikwa pamoja na babaze katika mji wa Daudi; na Hezekia mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 17

1 Katika mwaka wa kumi na mbili wa Ahazi mfalme wa Yuda Hoshea mwana wa Ela alianza kutawala juu ya Israeli katika Samaria; akatawala miaka kenda. 2 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, ila si kama wafalme wa Israeli waliomtangulia. 3 Naye Shalmanesa mfalme wa Ashuru akakwea juu yake, Hoshea akawa mtumishi wake, akampa kodi. 4 Mfalme wa Ashuru akaona fitina katika huyo Hoshea; kwa maana alikuwa ametuma wajumbe kwa So, mfalme wa Misri, wala hakumletea kodi mfalme wa Ashuru, kama alivyofanya mwaka kwa mwaka; kwa hiyo mfalme wa Ashuru akamfunga, akamtia kifungoni. 5 Ndipo mfalme wa Ashuru akakwea katikati ya nchi yote, akaenda Samaria, akauhusuru miaka mitatu. 6 Katika mwaka wa kenda wa Hoshea, huyo mfalme wa Ashuru akautwaa Samaria, akawahamisha Israeli mpaka Ashuru, akawaweka katika Hala na Habori, karibu na mto wa Gozani, na katika miji ya Wamedi. 7 Yalitukia hayo kwa sababu wana wa Israeli walikuwa wametenda dhambi juu ya Bwana, Mungu wao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri watoke chini ya mkono wa Farao mfalme wa Misri, wakawaacha miungu mingine. 8 Wakaziendea sheria za mataifa, ambao Bwana aliwafukuza mbele ya wana wa Israeli, na sheria za wafalme wa Israeli walizozifanya. 9 Tena, wana wa Israeli wakafanya kwa siri mambo yasiyokuwa mema juu ya Bwana, Mungu wao, wakajijengea mahali pa juu katika miji yao yote, kutoka mnara wa walinzi hata katika miji yenye boma. 10 Wakajisimamishia nguzo na maashera juu ya kila mlima mrefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi; 11 wakafukiza uvumba huko katika kila mahali pa juu, kama mataifa walivyofanya, ambao Bwana aliwafukuza mbele yao; wakaunda mambo mabaya, ili wamkasirishe Bwana; 12 wakatumikia sanamu, ambazo Bwana aliwakataza, akasema, Msitende jambo hili. 13 Pamoja na hayo Bwana aliwashuhudia Israeli, na Yuda, kwa kinywa cha kila nabii, na cha kila mwonaji, akisema, Geukeni, na kuziacha njia zenu mbaya, mkazishike amri zangu na hukumu zangu, sawasawa na ile sheria yote niliyowaamuru baba zenu, nikawapelekea kwa kinywa cha manabii watumishi wangu. 14 Walakini hawakutaka kusikia, bali walifanya shingo zao kuwa ngumu, kama shingo za baba zao, wasiomwamini Bwana, Mungu wao. 15 Wakazikataa sheria zake, na agano lake, alilolifanya na baba zao; na shuhuda zake alizowashuhudia; wakafuata ubatili, wakawa ubatili, nao wakaandamana na mataifa waliowazunguka, ambao Bwana alikuwa amewaagiza, wasitende kwa mfano wao. 16 Wakaziacha amri zote za Bwana, Mungu wao, wakajifanyizia sanamu za kusubu, yaani, ndama mbili, wakafanya na Ashera, wakaliabudu jeshi lote la mbinguni, wakamtumikia Baali. 17 Wakawapitisha watoto wao, waume na wake, motoni, wakapiga ramli, wakafanya uchawi, wakajiuza nafsi zao wapate kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, hata kumkasirisha. 18 Kwa hiyo Bwana akawaghadhibikia Israeli sana, akawahamisha mbali na uso wake; wala hapana aliyesalia ila kabila ya Yuda peke yake. 19 Hata na watu wa Yuda hawakuyashika maagizo ya Bwana, Mungu wao, lakini walikwenda katika amri za Israeli walizokuwa wamezifanya wenyewe. 20 Basi Bwana akakikataa kizazi chote cha Israeli, akawatesa, na kuwatia katika mikono ya watu wenye kuwateka nyara, hata alipokwisha kuwatupa, watoke machoni pake. 21 Maana aliwatenga mbali Israeli na nyumba ya Daudi; nao wakamfanya Yeroboamu mwana wa Nebati kuwa mfalme; Yeroboamu akawavuta Israeli wasimfuate Bwana, akawakosesha kosa kubwa. 22 Nao wana wa Israeli wakaendelea katika dhambi zote za Yeroboamu alizozifanya; hawakujiepusha nazo; 23 hata Bwana akawaondoa Waisraeli wasiwe mbele zake, kama vile alivyosema kwa kinywa cha watumishi wake wote, manabii. Basi Waisraeli walichukuliwa mateka kutoka nchi yao wenyewe, waende nchi ya Ashuru, hata leo. 24 Naye mfalme wa Ashuru akaleta watu kutoka Babeli, na Kutha, na Ava, na Hamathi, na Sefarvaimu, akawaweka katika miji ya Samaria badala ya wana wa Israeli; wakaumiliki Samaria, wakakaa katika miji yake. 25 Basi ikawa, wakati ule walipoanza kukaa huko, hawakumcha Bwana; kwa hiyo Bwana akapeleka simba kati yao, nao wakawaua baadhi yao. 26 Kwa hiyo wakamwambia mfalme wa Ashuru, wakasema, Wale wa mataifa uliowahamisha, na kuwaweka katika miji ya Samaria, hawaijui kawaida ya Mungu wa nchi; kwa hiyo amepeleka simba kati yao, na tazama, wanawaua, kwa sababu hawaijui kawaida ya Mungu wa nchi. 27 Ndipo mfalme wa Ashuru akatoa amri, akasema, Mpelekeni mmojawapo wa makuhani, mliowachukua kutoka huko; aende akakae huko, akawafundishe kawaida ya Mungu wa nchi. 28 Basi mmoja wa makuhani waliochukuliwa kutoka Samaria akaenda akakaa katika Betheli, akawafundisha jinsi ilivyowapasa kumcha Bwana. 29 Lakini pamoja na hayo watu wa kila taifa wakajifanyia miungu yao wenyewe, wakaiweka katika nyumba za mahali pa juu, walipopafanya Wasamaria, kila taifa katika miji yao walimokaa. 30 Watu wa Babeli wakafanya Sukoth-benothi kuwa mungu wao, watu wa Kutha wakafanya Nergali, watu wa Hamathi wakafanya Ashima, 31 Waavi wakafanya Nibhazi na Tartaki; nao Wasefarvi wakawaunguza wana wao katika moto kwa Adrameleki na Anameleki, miungu ya Sefarvaimu. 32 Basi hivyo wakamcha Bwana, nao wakijifanyia wengine wao kuwa makuhani wa mahali pa juu, ambao waliwafanyia dhabihu katika nyumba za mahali pa juu. 33 Wakamcha Bwana, na kuitumikia miungu yao wenyewe, sawasawa na kawaida za mataifa ambao wao walihamishwa kutoka kwao. 34 Hata siku hii ya leo hufanya sawasawa na kawaida za kwanza; wala hawamwogopi Bwana, wala hawazifuati sheria zao, wala hukumu zao, wala ile torati, wala ile amri Bwana aliyowaamuru wana wa Yakobo, ambaye alimpa jina la Israeli; 35 hao ambao Bwana alifanya agano nao, akawaamuru, akasema, Msiche miungu mingine, wala kuisujudia, wala kuitumikia, wala kuitolea sadaka; 36 ila yeye Bwana, aliyewaleta kutoka nchi ya Misri kwa nguvu nyingi, na kwa mkono ulionyoshwa, yeye ndiye mtakayemcha, yeye ndiye mtakayemsujudia, yeye ndiye mtakayemtolea sadaka; 37 na sheria, na hukumu, na torati, na amri, alizowaandikia, hizo ndizo mtakazozishika na kuzifanya hata milele; wala msiche miungu mingine. 38 Na hilo agano nililofanya nanyi, msilisahau; wala msiche miungu mingine; 39 lakini Bwana, Mungu wenu, ndiye mtakayemcha; naye atawaokoa mikononi mwa adui zenu wote. 40 Walakini hawakusikia, bali wakafanya sawasawa na kawaida zao za kwanza. 41 Basi mataifa hawa wakamcha Bwana, tena wakaziabudu sanamu zao za kuchongwa; na wana wao vile vile, na wana wa wana wao; kama walivyofanya baba zao, wao nao hufanya vivyo hivyo hata leo.

2 Wafalme 18

1 Ikawa katika mwaka wa tatu wa Hoshea, mwana wa Ela, mfalme wa Israeli, Hezekia, mwana wa Ahazi, mfalme wa Yuda, alianza kutawala. 2 Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka ishirini na kenda katika Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Abiya, binti Zekaria. 3 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, mfano wa yote aliyoyafanya Daudi, baba yake. 4 Alipaondoa mahali pa juu, akazibomoa nguzo, akaikata hiyo Ashera; akaivunja vipande vipande ile nyoka ya shaba aliyoifanya Musa; maana hata siku zile wana wa Israeli walikuwa wakiifukizia uvumba; naye akaiita jina lake Nehushtani 5 Alimtumaini Bwana, Mungu wa Israeli; hata baada yake hapakuwa na mfano wake katika wafalme wote wa Yuda, wala katika hao waliomtangulia. 6 Maana alishikamana na Bwana, hakuacha kumfuata, bali alizishika amri zake Bwana alizomwamuru Musa. 7 Naye Bwana akawa pamoja naye, kila alikokwenda alifanikiwa; tena alimwasi mfalme wa Ashuru, wala hakumtumikia. 8 Akawapiga Wafilisti mpaka Gaza na mipaka yake, tangu mnara wa walinzi hata mji wenye boma. 9 Hata katika mwaka wa nne wa Hezekia, ndio mwaka wa saba wa Hoshea, mwana wa Ela, mfalme wa Israeli, Shalmanesa, mfalme wa Ashuru, akakwea ili kupigana na Samaria, akauhusuru. 10 Wakautwaa baada ya miaka mitatu; yaani, katika mwaka wa sita wa Hezekia, ndio mwaka wa kenda wa Hoshea, mfalme wa Israeli, ndipo Samaria ulipotwaliwa. 11 Mfalme wa Ashuru akawahamisha Israeli mpaka Ashuru, akawaweka katika Hala, na katika Habori, karibu na mto wa Gozani, na katika miji ya Wamedi; 12 kwa sababu hawakuitii sauti ya Bwana, Mungu wao, bali waliyahalifu maagano yake, mambo yote ambayo Musa mtumishi wa Bwana aliwaamuru, wasikubali kuyasikiliza, wala kuyatenda. 13 Ikawa katika mwaka wa kumi na nne wa kumiliki kwake mfalme Hezekia, Senakeribu, mfalme wa Ashuru, akapanda ili kupigana na miji yote ya Yuda yenye boma, akaitwaa. 14 Basi Hezekia, mfalme wa Yuda, akapeleka wajumbe waende Lakishi kwa mfalme wa Ashuru, kusema, Nimekosa; uniache ukarudi kwako; cho chote utakachoweka juu yangu, nitakichukua. Mfalme wa Ashuru akamtoza Hezekia, mfalme wa Yuda, talanta za fedha mia tatu, na talanta za dhahabu thelathini. 15 Hezekia akampa fedha yote iliyoonekana katika nyumba ya Bwana, na katika hazina za nyumba ya mfalme. 16 Wakati huo Hezekia aliiondoa dhahabu iliyokuwa juu ya milango ya hekalu la Bwana, na juu ya nguzo, ambazo Hezekia, mfalme wa Yuda, alikuwa amezitia dhahabu, akampa mfalme wa Ashuru. 17 Mfalme wa Ashuru akawatuma jemadari wake, na mkuu wa matowashi, na amiri wake toka Lakishi ,kwa mfalme Hezekia huko Yerusalemu, pamoja na jeshi kubwa. Nao wakakwea wakafika Yerusalemu. Na walipokwisha kufika , wakaja wakasimama karibu na mfereji wa birika la juu, lililo katika njia kuu ya kuuendea uwanda wa dobi. 18 Na walipokwisha kumwita mfalme, wakatokewa na Eliakimu, mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba ya mfalme, na Shebna, mwandishi, na Yoa, mwana wa Asafu, mwenye kuandika tarehe. 19 Yule amiri akawaambia ,haya mwambieni Hezekia,kusema ,Mfalme mkuu,mfalme wa Ashuru, asema hivi, Ni tumaini gani hili unalolitumainia? 20 Wewe wasema, lakini ni maneno yasiyo na maana, kwamba, Lipo shauri na zipo nguvu kwa vita hivi. Basi, unamtumaini nani hata ukaniasi mimi? 21 Sasa tazama, unaitumainia fimbo ya mwanzi huu uliopondeka, yaani, Misri, ambayo mtu akiitegemea, humwingia mkononi na kumchoma; ndivyo alivyo Farao, mfalme wa Misri, kwa wote wamtumainio. 22 Lakini mkiniambia, Tunamtumaini Bwana, Mungu wetu; je! Si yeye ambaye Hezekia ameondoa mahali pake pa juu, na madhabahu zake, akawaambia watu wa Yuda na Yerusalemu, Sujuduni mbele ya madhabahu hii hapa Yerusalemu? 23 Basi sasa, tafadhali mpe bwana wangu, mfalme wa Ashuru, dhamana, nami nitakupa farasi elfu mbili, ikiwa wewe kwa upande wako waweza kupandisha watu juu yao. 24 Wawezaje, basi, kurudisha nyuma uso wa akida mmoja wa watumishi walio wadogo wa bwana wangu, na kuitumainia Misri upewe magari na farasi? 25 Je! Nimepanda mimi, ili kupigana na mahali hapa na kupaangamiza, bila shauri la Bwana? Bwana ndiye aliyeniambia, Panda upigane na nchi hii na kuiangamiza. 26 Ndipo Eliakimu, mwana wa Hilkia, na Shebna, na Yoa, wakamwambia yule amiri, Tafadhali, sema na watumishi wako kwa lugha ya Kiashuri; maana tunaifahamu; wala usiseme nasi kwa lugha ya Kiyahudi, masikioni mwa hao watu walio ukutani. 27 Lakini yule amiri akawaambia, Je! Bwana wangu amenituma kwa bwana wako, na kwako wewe, niseme maneno haya? Je! Hakunituma kwa watu hawa walio ukutani, ili wale mavi yao wenyewe na kunywa mkojo wao pamoja nanyi? 28 Kisha yule amiri akasimama akalia kwa sauti kuu kwa lugha ya Kiyahudi, akasema, Lisikieni neno la mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru. 29 Mfalme asema hivi, Hezekia asiwadanganye; kwa maana, hataweza kuwaokoa katika mkono wake. 30 Wala Hezekia asiwatumainishe katika Bwana, akisema, Hakika Bwana atatuokoa, wala mji huu hautatiwa mkononi mwa mfalme wa Ashuru. 31 Msimsikilize Hezekia; kwa sababu mfalme wa Ashuru asema hivi, Fanyeni suluhu na mimi, mkatoke mnijie; mkale kila mtu matunda ya mzabibu wake na matunda ya mtini wake, mkanywe kila mmoja maji ya birika lake mwenyewe; 32 hata nije nikawachukue mpaka nchi iliyo kama nchi yenu wenyewe, nchi ya nafaka na divai, nchi ya chakula na mashamba ya mizabibu, nchi ya mafuta ya mzeituni na asali, ili mpate kuishi, msife; wala msimsikilize Hezekia, awadanganyapo, akisema, Bwana atatuokoa. 33 Je! Yuko mungu mmoja wa mataifa aliyewaokoa watu wake wakati wo wote na mkono wa mfalme wa Ashuru? 34 Iko wapi miungu ya Hamathi, na ya Arpadi? Iko wapi miungu ya Sefarvaimu, na ya Hena, na ya Iva? Je! Imeuokoa Samaria na mkono wangu? 35 Katika miungu ya nchi hizi zote, ni miungu gani iliyookoa nchi yao na mkono wangu, hata Bwana auokoe Yerusalemu na mkono wangu? 36 Lakini hao watu wakanyamaza kimya; wala hawakumjibu hata neno moja; maana amri ya mfalme ilikuwa kwamba, Msimjibu neno. 37 Ndipo Eliakimu, mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba ya mfalme, na Shebna, mwandishi, na Yoa, mwana wa Asafu, mwenye kuandika tarehe, wakaenda kwa Hezekia, na nguo zao zimeraruliwa, wakamwambia maneno ya yule amiri.

2 Wafalme 19

1 Ikawa mfalme Hezekia aliposikia hayo, alizirarua nguo zake, akajivika nguo za magunia, akaingia katika nyumba ya Bwana. 2 Akamtuma Eliakimu aliyekuwa msimamizi wa nyumba yake na Shebna, mwandishi, na wazee wa makuhani, wamevikwa nguo za magunia, waende kwa Isaya nabii, mwana wa Amozi. 3 Wakamwambia, Hezekia asema hivi, Siku hii ni siku ya dhiki, na aibu, na matukano; maana watoto wa tayari kuzaliwa, wala hapana nguvu za kuwazaa. 4 Yamkini Bwana, Mungu wako, atayasikia maneno yote ya amiri huyu, ambaye mfalme wa Ashuru ,bwana wake,amemtuma ili amtukane Mungu aliye hai,naye atayakemea hayo maneno aliyoyasikia BWANA ,Mungu wako;kwa sababu hii inua dua yako kwa ajili ya mabaki yaliyobakia. 5 Basi watumishi wa mfalme Hezekia wakamwendea Isaya. 6 Isaya akawaambia, Mwambieni bwana wenu maneno haya; Bwana asema hivi, Usiyaogope maneno hayo uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mfalme wa Ashuru wamenitukana. 7 Tazama, nitatia roho ya hofu ndani yake, naye atasikia kivumi, na kuirudia nchi yake mwenyewe; nami nitamwangusha kwa upanga katika nchi yake mwenyewe. 8 Basi yule amiri akarudi, akamkuta mfalme wa Ashuru, anapigana na Libna; maana alikuwa amesikia ya kwamba ameondoka, akaacha Lakishi. 9 Na aliposikia habari ya Tirhaka mfalme wa Kushi, ya kwamba, Tazama, ametoka ili kupigana nawe; alituma wajumbe kwa Hezekia mara ya pili, kusema, 10 Mwambieni Hezekia, mfalme wa Yuda, maneno haya, mkisema, Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru. 11 Tazama, umesikia ni mambo gani wafalme wa Ashuru waliyozitenda nchi zote, kwa kuziangamiza kabisa; je! Utaokoka wewe? 12 Je! Miungu ya mataifa wale, ambao baba zangu waliwaangamiza, imewaokoa? Yaani, Gozani, na Harani, na Resefu, na wana wa Adini waliokuwa katika Telasari? 13 Yuko wapi mfalme wa Hamathi, na mfalme wa Arpadi, na mfalme wa mji wa Sefarvaimu, na wa Hena, na wa Iva? 14 Basi Hezekia akaupokea waraka katika mikono ya wale wajumbe, akausoma; kisha Hezekia akapanda, akaingia katika nyumba ya Bwana, akaukunjua mbele za Bwana. 15 Naye Hezekia akaomba mbele za Bwana, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia; wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi. 16 Tega sikio lako, Ee Bwana, usikie; fumbua macho yako, Ee Bwana, uone; uyasikie maneno ya Senakeribu, ambayo amemtuma mtu aje nayo ili kumtukana Mungu aliye hai. 17 Ni kweli, Bwana, wafalme wa Ashuru wamewaharibu mataifa na nchi zao, 18 na kuitupa miungu yao motoni; kwa maana haikuwa miungu, bali ni kazi ya mikono ya wanadamu; ilikuwa miti na mawe tu, ndiyo sababu wakaiharibu. 19 Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, nakusihi, ili kwamba falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe Bwana Mungu, wewe peke yako. 20 Ndipo Isaya, mwana wa Amozi, akapeleka ujumbe kwa Hezekia, akisema, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa kuwa umeniomba juu ya Senakeribu, mfalme wa Ashuru, mimi nimekusikia. 21 Tamko alilolitamka Bwana katika habari zake ndilo hili, Bikira, binti Sayuni, amekudharau, na kukudhihaki sana; binti Yerusalemu ametikisa kichwa chake juu yako. 22 Ni nani uliyemshutumu na kumtukana? Umeinua sauti yako juu ya nani, na kuinua macho yako juu? Juu ya Mtakatifu wa Israeli. 23 Kwa vinywa vya wajumbe wako umemshutumu Bwana, ukasema, Kwa wingi wa magari yangu nimepanda juu ya vilele vya milima, mpaka mahali pa ndani pa Lebanoni. Nami nitaikata mierezi yake mirefu, na misunobari yake mizuri; nami nitaingia ndani ya makazi yake yaliyo mbali sana, na msitu wa shamba lake lizaalo sana. 24 Nimechimba na kunywa maji mageni, na kwa nyayo za miguu yangu nitaikausha mito yote ya Misri. 25 Je! Hukusikia wewe ya kuwa mimi ndimi niliyeyatenda hayo tokea zamani, na kuyafanya tokea siku za kale? Sasa mimi nimelitimiza jambo hili, iwe kazi yako kuangamiza miji yenye boma, hata ikawe chungu na magofu. 26 Ndiyo sababu wenyeji wao walikuwa na nguvu chache, wakafadhaika, na kuhangaika; wakawa kama majani ya mashamba, kama miche mibichi, kama majani juu ya dari, na kama ngano iliyokaushwa kabla haijaiva. 27 Lakini nakujua, kuketi kwako, na kutoka kwako, na kuingia kwako; na ghadhabu yako unayonighadhibikia. 28 Kwa sababu ya kunighadhibikia kwako, na kwa sababu kutakabari kwako kumefika masikioni mwangu; kwa sababu hiyo nitatia kulabu yangu puani mwako, na hatamu yangu midomoni mwako, nami nitakurudisha nyuma kwa njia ile ile uliyoijia. 29 Na kwako wewe hii ndiyo dalili; mwaka huu mtakula vitu viotavyo vyenyewe; na mwaka wa pili mtakula mazao ya vitu hivyo; na mwaka wa tatu pandeni mbegu, kavuneni; mkapande mashamba ya mizabibu, mkale matunda yake. 30 Na mabaki yaliyookoka ya nyumba ya Yuda yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu. 31 Maana mabaki yatatoka katika Yerusalemu, na wao watakaookoka katika mlima wa Sayuni wivu wa Bwana utatimiza jambo hilo. 32 Basi Bwana asema hivi katika habari za mfalme wa Ashuru, Yeye hatauingia mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hatakuja mbele yake kwa ngao, wala hatajenga boma juu yake. 33 Njia ile ile aliyojia, kwa njia iyo hiyo atarudi zake, wala hataingia ndani ya mji huu, asema Bwana. 34 Maana nitaulinda mji huu, niuokoe, kwa ajili yangu mwenyewe, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu. 35 Ikawa usiku uo huo malaika wa Bwana alitoka, akakiingia kituo cha Waashuri, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu. Na watu walipoondoka asubuhi na mapema, kumbe! Hao walikuwa maiti wote pia. 36 Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda zake, akarudi akakaa Ninawi. 37 Ikawa, alipokuwa akiabudu nyumbani mwa Nisroki, mungu wake, Adrameleki na Shareza wakampiga kwa upanga; wakaikimbilia nchi ya Ararati. Na Esar-hadoni mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 20

1 Siku hizo Hezekia akaugua, akawa katika hatari ya kufa. Isaya, nabii, mwana wa Amozi, akamjia akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. 2 Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana akasema, 3 Nakusihi, Bwana, ukumbuke sasa, jinsi nilivyokwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. 4 Ikawa, kabla Isaya hajatoka katika mji wa kati, neno la Bwana likamjia, kusema, 5 Rudi, ukamwambie Hezekia, mkuu wa watu wangu, Bwana, Mungu wa Daudi baba yako asema hivi, Nimeyasikia maombi yako, na kuyaona machozi yako; tazama, nitakuponya; siku ya tatu utapanda nyumbani kwa Bwana. 6 Tena, nitazizidisha siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano, nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu. 7 Naye Isaya akasema, Twaeni mkate wa tini. Wakautwaa, wakauweka juu ya jipu, naye akapona. 8 Hezekia akamwambia Isaya, Je! Kutakuwa na ishara gani ya kwamba Bwana ataniponya, nami siku ya tatu nitapanda nyumbani kwa Bwana. 9 Isaya akamwambia, Jambo hili litakuwa ishara kwako, itokayo kwa Bwana, ya kwamba Bwana atalifanya neno hilo alilolinena; je! Kivuli kiendelee madaraja kumi, au kirudi nyuma madaraja kumi? 10 Hezekia akajibu, Ni jambo jepesi kivuli kuendelea madaraja kumi; la, hicho kivuli na kirudi nyuma madaraja kumi. 11 Isaya nabii akamlilia Bwana; akakirudisha nyuma kile kivuli madaraja kumi, ambayo kilikuwa kimeshuka katika madaraja ya Ahazi. 12 Wakati huo Merodak-baladani mwana wa Baladani, Mfalme wa Babeli, alipeleka barua na zawadi kwa Hezekia; kwa maana alipata habari kwamba Hezekia ameugua. 13 Hezekia akawasikiliza, akawaonyesha nyumba yote yenye vitu vyake vya thamani, fedha, na dhahabu, na manukato, na marhamu ya thamani, na nyumba yenye silaha zake, na vitu vyote vilivyoonekana katika hazina zake. Wala hapakuwa na kitu asichowaonyesha Hezekia, katika nyumba yake, wala katika ufalme wake wote. 14 Ndipo Isaya nabii akamwendea mfalme Hezekia, akamwambia, Wasemaje watu hawa? Nao wametoka wapi kuja kwako? Hezekia akasema, Wametoka katika nchi iliyo mbali, yaani Babeli. 15 Ndipo akasema, Wameona nini nyumbani mwako? Hezekia akajibu, Vitu vyote vilivyomo nyumbani mwangu wameviona; hapana kitu nisichowaonyesha katika hazina zangu. 16 Isaya akamwambia Hezekia, Basi, lisikie neno la Bwana, 17 Angalia, siku zinakuja, ambazo vitu vyote vilivyomo nyumbani mwako, na hivyo vilivyowekwa akiba na baba zako hata leo, vitachukuliwa mpaka Babeli; hakitasalia kitu, asema Bwana. 18 Na baadhi ya wanao watakaotoka kwako, utakaowazaa, watawachukulia mbali; nao watakuwa matowashi jumbani mwake mfalme wa Babeli. 19 Ndipo Hezekia akamwambia Isaya, Neno la Bwana ulilolinena ni jema. Tena akasema, Je! Sivyo, ikiwapo amani na kweli katika siku zangu? 20 Basi mambo yote ya Hezekia yaliyosalia, na ushujaa wake wote, tena alivyolifanya birika na mfereji, akaleta maji ndani ya mji, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 21 Hezekia akalala na baba zake; na Manase mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 21

1 Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala; akatawala miaka hamsini na mitano katika Yerusalemu, na jina la mamaye aliitwa Hefziba. 2 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, sawasawa na machukizo ya mataifa, aliowafukuza Bwana mbele ya wana wa Israeli. 3 Kwa maana akapajenga tena mahali pa juu alipopaharibu Hezekia baba yake; akamjengea Baali madhabahu, akafanya Ashera kama alivyofanya Ahabu mfalme wa Israeli. Akajiinama mbele ya jeshi lote la mbinguni na kulitumikia. 4 Akazijenga madhabahu ndani ya nyumba ya Bwana, napo ndipo alipopanena Bwana, Katika Yerusalemu nitaliweka jina langu. 5 Akajenga madhabahu kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni katika behewa mbili za nyumba ya Bwana. 6 Akampitisha mwanawe motoni, akatazama bao, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa Bwana, hata kumkasirisha. 7 Akaiweka sanamu ya kuchongwa ya Ashera aliyoifanya ndani ya nyumba, ambayo Bwana alimwambia Daudi, na Sulemani mwanawe, Katika nyumba hii, na katika Yerusalemu, niliouchagua miongoni mwa kabila zote za Israeli, nitaliweka jina langu milele; 8 wala sitawapotosha Israeli miguu watoke katika nchi niliyowapa baba zao; wakiangalia tu na kufanya sawasawa na yote niliyowaamuru, na kwa kuishika torati yote aliyowaamuru mtumishi wangu Musa. 9 Walakini hawakusikia; naye Manase akawakosesha wafanye mabaya, kuliko mataifa Bwana aliowaharibu mbele za wana wa Israeli. 10 Bwana akanena kwa watumishi wake manabii, akisema, 11 Kwa sababu Manase mfalme wa Yuda amefanya machukizo haya, na kutenda vibaya kuliko yote waliyoyatenda Waamori, waliokuwa kabla yake, naye akawakosesha Yuda kwa sanamu zake; 12 kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Angalia, naleta mabaya juu ya Yerusalemu na juu ya Yuda, hata kila mtu asikiaye, masikio yake yatawasha yote mawili. 13 Nami nitanyosha juu ya Yerusalemu kamba ya Samaria, na timazi ya nyumba ya Ahabu; nami nitaifuta Yerusalemu, kama mtu afutavyo sahani, kuifuta na kuifudikiza. 14 Nami nitawatupa mabaki ya urithi wangu, na kuwatia mikononi mwa adui zao; nao watakuwa nyara na mateka kwa adui zao wote; 15 kwa sababu wametenda yaliyo mabaya machoni pangu, na kunikasirisha, tangu siku ile walipotoka baba zao katika Misri, hata leo hivi. 16 Na Manase akazimwaga damu zisizo na hatia, nyingi sana, hata alipokuwa ameijaza Yerusalemu tangu upande huu hata upande huu; zaidi ya kosa lake alilowakosesha Yuda, kutenda yaliyo mabaya machoni pa Bwana. 17 Basi mambo yote ya Manase yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, na kosa lake alilolikosa, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 18 Manase akalala na babaze, akazikwa katika bustani ya nyumba yake mwenyewe, yaani, bustani ya Uza. Na Amoni mwanawe akatawala mahali pake. 19 Amoni alikuwa na umri wa miaka ishirini na miwili alipoanza kutawala; akatawala miaka miwili huko Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Meshulemethi, binti Haruzi wa Yotba. 20 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, kama Manase babaye alivyofanya. 21 Akaiendea njia yote aliyoiendea baba yake, akazitumikia sanamu alizozitumikia baba yake, akaziabudu. 22 Akamwacha Bwana, Mungu wa babaze, wala hakuiendea njia ya Bwana. 23 Nao watumishi wa Amoni wakafanya fitina juu yake, wakamwua mfalme ndani ya nyumba yake mwenyewe. 24 Lakini watu wa nchi wakawaua wote waliofanya fitina juu yake mfalme Amoni, watu wa nchi wakamfanya Yosia mwanawe awe mfalme mahali pake. 25 Basi mambo yote ya Amoni yaliyosalia, aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 26 Akazikwa kaburini mwake katika bustani ya Uza. Na Yosia mwanawe akatawala mahali pake.

2 Wafalme 22

1 Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala; akatawala miaka thelathini na mmoja katika Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Yedida, binti Adaya wa Bozkathi. 2 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, akaenda katika njia yote ya Daudi baba yake, wala hakugeuka upande wa kuume wala wa kushoto. 3 Ikawa, katika mwaka wa kumi na nane wa mfalme Yosia, mfalme akamtuma Shafani, mwana wa Azalia, mwana wa Meshulamu, mwandishi, nyumbani kwa Bwana, akisema, 4 Enenda kwa Hilkia, kuhani mkuu, ili aihesabu fedha yote inayoletwa nyumbani mwa Bwana, ambayo mabawabu wameipokea kwa watu; 5 tena waitie ile fedha katika mikono ya wafanya kazi wanaoisimamia nyumba ya Bwana; wakapewe wafanya kazi waliomo ndani ya nyumba ya Bwana, ili wapate kupatengeneza mahali palipobomoka ndani ya nyumba; 6 wapewe maseremala, na wajenzi, na waashi; ili kununua miti na mawe yaliyochongwa wapate kuitengeneza nyumba. 7 Lakini hawakuulizwa habari za ile fedha waliyokabidhiwa; maana walitenda kazi kwa uaminifu. 8 Naye Hilkia, kuhani mkuu, akamwambia Shafani, mwandishi, Nimekiona kitabu cha torati katika nyumba ya Bwana. Hilkia akampa Shafani kile kitabu, naye akakisoma. 9 Shafani mwandishi akamwendea mfalme, akamletea mfalme habari tena, akasema, Watumishi wako wamezitoa zile fedha zilizoonekana ndani ya nyumba, nao wamewakabidhi wafanya kazi wanaoisimamia nyumba ya Bwana. 10 Kisha Shafani mwandishi akamwambia mfalme, akasema, Hilkia kuhani amenipa kitabu. Shafani akakisoma mbele ya mfalme. 11 Ikawa, mfalme alipokwisha kuyasikia maneno ya kitabu hicho cha torati, alirarua nguo zake. 12 Mfalme akamwamuru Hilkia kuhani, na Ahikamu, mwana wa Shafani, na Akbori, mwana wa Mikaya, na Shafani mwandishi, na Asaya, mtumishi wa mfalme akasema, 13 Enendeni, mkamwulize Bwana kwa ajili yangu, na kwa ajili ya watu hawa, na kwa ajili ya Yuda yote, katika habari za maneno ya kitabu hiki kilichoonekana; kwa kuwa hasira ya Bwana ni kubwa aliyotukasirikia, kwa sababu baba zetu hawakuyaangalia maneno ya kitabu hiki, kufanya kama hayo yote tuliyoandikiwa. 14 Basi Hilkia kuhani, na Ahikamu, na Akbori, na Shafani, na Asaya, wakamwendea Hulda, nabii mke, mkewe Shalumu, mwana wa Tikva, mwana wa Harhasi, mtunza mavazi ya mfalme; (naye alikaa Yerusalemu katika mtaa wa pili;) wakasema naye. 15 Akawaambia, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Mwambieni mtu yule aliyewatuma ninyi kwangu, 16 Bwana asema hivi, Tazama, mimi nitaleta uovu juu ya mahali hapa, na juu yao wakaao hapa, naam, maneno yote ya kitabu alichokisoma mfalme wa Yuda; 17 kwa sababu wameniacha mimi, wameifukizia uvumba miungu mingine, ili wapate kunikasirisha kwa kazi yote ya mikono yao; kwa hiyo hasira yangu itawaka juu ya mahali hapa, isizimike. 18 Lakini yule mfalme wa Yuda, aliyewatuma ninyi kumwuliza Bwana, mtamwambia hivi, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa habari ya maneno yale uliyoyasikia, 19 kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe ukajinyenyekesha mbele za Bwana, hapo ulipoyasikia maneno niliyoyanena juu ya mahali hapa, na juu ya wenyeji wake, ya kwamba watakuwa ukiwa na laana, nawe ulizirarua nguo zako, ukalia mbele zangu; basi, mimi nami nimekusikia wewe, asema Bwana. 20 Kwa hiyo tazama, nitakukusanya pamoja na baba zako, nawe utawekwa kaburini mwako kwa amani; wala macho yako hayatauona uovu huo wote nitakaouleta juu ya mahali hapa. Basi wakamletea mfalme habari tena.

2 Wafalme 23

1 Kisha, mfalme akatuma wajumbe, nao wakamkusanyia wazee wote wa Yuda na wa Yerusalemu. 2 Mfalme akapanda kwenda nyumbani kwa Bwana, na watu wote wa Yuda, nao wote waliokaa Yerusalemu, pamoja naye, na makuhani, na manabii, na watu wote, wadogo kwa wakubwa; akasoma masikioni mwao maneno yote ya kitabu cha agano kilichoonekana katika nyumba ya Bwana. 3 Mfalme akasimama karibu na nguzo, akafanya agano mbele za Bwana, kumfuata Bwana, na kuyashika maagizo yake, na shuhuda zake, na amri zake, kwa moyo wake wote, na kwa roho yake yote, na kuyathibitisha maneno ya agano hilo yaliyoandikwa katika kitabu hicho; nao watu wote wakalikubali agano lile. 4 Kisha, mfalme akamwamuru Hilkia, kuhani mkuu, na makuhani wa daraja ya pili, na walinzi wa mlango, kwamba watoe katika hekalu la Bwana vyombo vyote vilivyofanywa kwa ajili ya Baali, na kwa ajili ya Ashera, na kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni; akavipiga moto nje ya Yerusalemu, katika mashamba ya Ridroni, akayachukua majivu yake mpaka Betheli. 5 Akawaondosha wale makuhuni walioabudu sanamu, ambao wafalme wa Yuda waliwaweka ili kufukiza uvumba katika mahali pa juu, ndani ya miji ya Yuda, na katika kila mahali, pande zote za Yerusalemu; na hao pia waliomfukizia uvumba Baali, na jua, na mwezi, na sayari, na jeshi lote la mbinguni. 6 Naye akaiondoa Ashera katika nyumba ya Bwana, nje ya Yerusalemu, mpaka Kidroni, akaipiga moto penye kijito cha Kidroni, na kuiponda-ponda iwe mavumbi, akayatupa mavumbi yake juu ya makaburi ya watu. 7 Akaziangusha nyumba za mahanithi, waliokuwamo nyumbani mwa Bwana, wanawake walipofuma mapazia ya Ashera. 8 Akawatoa makuhani wote katika miji ya Yuda, akapanajisi mahali pa juu, makuhani walipokuwa wamefukiza uvumba, tangu Geba hata Beer-sheba; akapavunja mahali pa juu pa malango, palipokuwapo penye kuingia lango la Yoshua, liwali wa mji, palipokuwa upande wa kushoto wa mtu langoni pa mji. 9 Walakini hao makuhani wa mahali pa juu hawakupanda madhabahuni kwa Bwana katika Yerusalemu, bali wakala mikate isiyo na chachu katikati ya ndugu zao. 10 Naye akainajisi Tofethi, iliyomo katika bonde la wana wa Hinomu, ili mtu asipitishe mwana wake au binti yake motoni kwa Moleki. 11 Akawaondoa farasi ambao wafalme wa Yuda waliwatoa kwa jua, hapo pa kuingia nyumbani mwa Bwana, karibu na chumba cha Nathan-Meleki, towashi, kilichohuwako kiungani; akayapiga moto magari ya jua. 12 Nazo madhabahu zilizokuwako darini juu ya chumba cha juu cha Ahazi, wafalme wa Yuda walizozifanya, nazo madhabahu alizozifanya Manase katika behewa mbili za nyumba ya Bwana, mfalme akazivunja, akazitelemsha huko nje, na kuyatupa mavumbi yake katika kijito cha Kidroni. 13 Na mahali pa juu palipokuwapo mbele ya Yerusalemu, palipokuwa upande wa kuume wa mlima wa uharibifu, alipopajenga Sulemani, mfalme wa Israeli, kwa Ashtorethi, chukizo la Wasidoni, na Kemoshi, chukizo la Moabu, na Milkomu, chukizo la wana wa Amoni, mfalme akapanajisi. 14 Akazivunja-vunja nguzo, akayakata-kata maashera, akapajaza mahali pake mifupa ya watu. 15 Tena zaidi ya hayo, ile madhabahu iliyokuwako Betheli, na mahali pa juu alipopafanya Yeroboamu, mwana wa Nebati, aliyewakosesha Israeli, madhabahu hiyo aliibomoa; na mahali pa juu alipateketeza, akapaponda-ponda hata pakawa mavumbi, akaiteketeza ile Ashera. 16 Naye Yosia alipogeuka, aliyaona makaburi yale yaliyokuwako huko, juu ya mlima; akatuma watu, akaitoa ile mifupa katika yale makaburi, akaiteketeza juu ya madhabahu, akainajisi, sawasawa na lile neno la Bwana, alilolinena yule mtu wa Mungu, aliyetamka mambo hayo. 17 Kisha akasema, Ni kumbukumbu la nani, hili ninaloliona? Na watu wa mji wakamwambia, Ni kaburi la yule mtu wa Mungu, aliyetoka Yuda, akayanena mambo hayo uliyoyatenda wewe juu ya madhabahu ya Betheli. 18 Akasema, Mwacheni; mtu awaye yote asiiondoe mifupa yake. Basi wakaiacha mifupa yake, pamoja na mifupa ya yule nabii aliyetoka Samaria. 19 Na nyumba zote pia za mahali pa juu palipokuwa katika miji ya Samaria, wafalme wa Israeli walizozifanya, ili kumkasirisha Bwana, Yosia aliziondoa, akazitenda kwa mfano wa mambo yote aliyoyatenda katika Betheli. 20 Akawaua na makuhani wote wa mahali pa juu waliokuwako huko, juu ya madhabahu, akateketeza mifupa ya watu juu yake; kisha akarejea Yerusalemu. 21 Naye mfalme akawaamuru watu wote, akasema, Mfanyieni Bwana, Mungu wenu, pasaka, kama ilivyoandikwa katika kitabu hiki cha agano. 22 Hakika yake haikufanyika pasaka kama hiyo, tangu zamani za waamuzi waliowaamua Israeli, wala katika zamani za wafalme wa Israeli, wala za wafalme wa Yuda. 23 Bali katika mwaka wa kumi na nane wa mfalme Yosia ilifanyika pasaka hii kwa Bwana ndani ya Yerusalemu. 24 Tena wenye pepo wa utambuzi, na wachawi, na vinyago, na sanamu, na machukizo yote yaliyoonekana katika nchi ya Yuda na katika Yerusalemu, Yosia akayaondoa yote, ili apate kuyathibitisha maneno ya torati yaliyoandikwa katika kile kitabu alichokiona Hilkia kuhani ndani ya nyumba ya Bwana. 25 Kabla ya huyo hapakuwa na mfalme mfano wake, aliyemwelekea Bwana kwa moyo wake wote, na kwa roho yake yote, na kwa nguvu zake zote, sawasawa na sheria zote za Musa; wala baada yake hakuinuka mmoja mfano wake yeye. 26 Walakini Bwana hakuuacha ukali wa ghadhabu yake nyingi, ambayo kwayo hasira yake iliwaka juu ya Yuda, kwa sababu ya machukizo yote ambayo Manase amemchukiza. 27 Bwana akasema Nitawahamisha Yuda pia mbali nami, kama nilivyowahamisha Israeli, nami nitautupa mji huu niliouchagua, naam, Yerusalemu, na nyumba ile niliyoinena, Jina langu litakuwa humo. 28 Basi mambo yote ya Yosia yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 29 Katika siku zake, Farao-neko, mfalme wa Misri, akakwea ili kupigana na mfalme wa Ashuru, akafika mto Frati; naye mfalme Yosia akaenda kupigana naye; naye mfalme wa Misri akamwua huko Megido, hapo alipoonana naye. 30 Watumishi wake wakamchukua garini, amekwisha kufa, kutoka Megido, wakamleta Yerusalemu, wakamzika katika kaburi lake mwenyewe. Watu wa nchi wakamtwaa Yehoahazi mwana wa Yosia, wakamtia mafuta, wakamtawaza awe mfalme badala ya baba yake. 31 Yehoahazi alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitatu alipoanza kutawala; akatawala miezi mitatu katika Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Hamutali binti Yeremia wa Libna. 32 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, sawasawa na yote waliyoyafanya baba zake. 33 Naye Farao-neko akamfunga huko Ribla, katika nchi ya Hamathi, ili asitawale huko Yerusalemu. Akaitoza nchi kodi talanta mia za fedha na talanta ya dhahabu. 34 Farao-neko akamfanya Eliakimu mwana wa Yosia awe mfalme mahali pa Yosia babaye, akambadilisha jina lake kuwa Yehoyakimu, lakini akamwondoa Yehoahazi; akaenda naye Misri, naye akafa huko. 35 Na Yehoyakimu akampa Farao dhahabu na fedha; lakini akaitoza nchi kodi, ili apate kutoa zile fedha kwa amri yake Farao; akawatoza fedha na dhahabu watu wa nchi, kila mtu kwa kodi yake, ili ampe Farao-neko. 36 Yehoyakimu alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka kumi na mmoja huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Zebida binti Pedaya wa Ruma. 37 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, sawasawa na yote waliyoyafanya baba zake.

2 Wafalme 24

1 Katika siku zake akakwea Nebukadreza, mfalme wa Babeli na Yehoyakimu akawa mtumishi wake muda wa miaka mitatu;kisha ,akageuka,akamwasi. 2 Naye Bwana akatuma juu yake vikosi vya Wakaldayo, na vikosi vya Washami, na vikosi vya Wamoabi, na vikosi vya wana wa Amoni, akawatuma juu ya Yuda ili kuiharibu, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa mkono wa watumishi wake manabii. 3 Hakika kwa amri ya Bwana mambo hayo yalimpata Yuda, ili waondoshwe kutoka machoni pake, kwa sababu ya dhambi zake Manase, kadiri ya yote aliyoyafanya; 4 tena kwa ajili ya damu zisizo na hatia alizozimwaga; kwani aliujaza Yerusalemu damu zisizo na hatia; wala Bwana hakukubali kusamehe. 5 Basi mambo yote ya Yehoyakimu yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda? 6 Yehoyakimu akalala na babaze; na mwanawe Yekonia akatawala mahali pake. 7 Basi mfalme wa Misri hakuja tena kutoka nchi yake; kwa kuwa mfalme wa Babeli alikuwa amemnyang'anya nchi, tangu kijito cha Misri mpaka mto wa Frati, yote aliyokuwa nayo mfalme wa Misri. 8 Yekonia alikuwa na umri wa miaka kumi na minane alipoanza kutawala; akatawala miezi mitatu katika Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Nehushta binti Elnathani wa Yerusalemu. 9 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, mfano wa yote aliyoyafanya baba yake. 10 Wakati ule watumishi wa Nebukadreza mfalme wa Babeli wakakwea kwenda Yerusalemu, na mji ukahusuriwa. 11 Na Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akaufikilia huo mji, hapo watumishi wake walipokuwa wakiuhusuru. 12 Na Yekonia, mfalme wa Yuda, akatoka akamwendea mfalme wa Babeli, yeye na mama yake, na watumishi wake, na wakuu wa watu wake, na maakida wake; mfalme wa Babeli akamchukua mateka katika mwaka wa nane wa kutawala kwake. 13 Akatoa huko hazina zote za nyumba ya Bwana, na hazina za nyumba ya mfalme, akavikata-kata vyombo vyote vya dhahabu ambavyo Sulemani, mfalme wa Israeli, alivifanya katika hekalu la Bwana, kama Bwana alivyosema. 14 Akawachukua mateka watu wa Yerusalemu wote pia, na wakuu wote, na mashujaa wote, watu elfu kumi; na mafundi wote, na wafua chuma wote; hapana mtu aliyebaki, ila waliokuwa wanyonge wa watu wa nchi. 15 Akamchukua Yekonia mpaka Babeli; na mama yake mfalme, na wake zake mfalme, na maakida wake, na wakuu wa nchi, aliwachukua mateka toka Yerusalemu mpaka Babeli. 16 Na mashujaa wote, watu elfu saba, na mafundi na wafua chuma elfu moja, wote pia wenye nguvu, tayari kwa vita, hao wote mfalme wa Babeli aliwachukua mateka mpaka Babeli. 17 Mfalme wa Babeli akamtawaza Matania, ndugu ya baba yake, awe mfalme badala yake, akalibadili jina lake, akamwita Sedekia. 18 Sedekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja alipoanza kutawala; akatawala miaka kumi na mmoja katika Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Hamutali, binti Yeremia wa Libna. 19 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyafanya Yehoyakimu. 20 Maana kwa sababu ya hasira ya Bwana mambo hayo yalitokea katika Yerusalemu na katika Yuda, hata alipokuwa amewaondosha wasiwe mbele ya uso wake; naye Sedekia akamwasi mfalme wa Babeli.

2 Wafalme 25

1 Ikawa katika mwaka wa kenda wa kutawala kwake, katika mwezi wa kumi, na siku ya kumi ya mwezi huo, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akaja, yeye na jeshi lake lote, kupigana na Yerusalemu, akapanga hema zake kuukabili; nao wakajenga ngome juu yake pande zote. 2 Basi mji huo ulihusuriwa hata mwaka wa kumi na moja wa mfalme Sedekia. 3 Siku ya kenda ya mwezi wa nne njaa ilikuwa nzito ndani ya mji, hata hapakuwa na chakula kwa watu wa nchi. 4 Ndipo mahali pakabomolewa katika ukuta wa mji, watu wote wa vita wakakimbia usiku kwa njia ya lango lililokuwa kati ya zile kuta mbili, karibu na bustani ya mfalme; (basi wale Wakaldayo walikuwa wakiuzuia mji pande zote;) mfalme akaenda kwa njia ya Araba. 5 Lakini jeshi la Wakaldayo wakamfuatia mfalme, wakampata katika nchi tambarare ya Yeriko; na jeshi lake lote walikuwa wametawanyika na kumwacha. 6 Ndipo wakamkamata mfalme, wakamchukua kwa mfalme wa Babeli huko Ribla; wakatoa hukumu juu yake. 7 Wakawaua wana wa Sedekia mbele ya macho yake, wakampofusha macho Sedekia, wakamfunga kwa pingu, wakamchukua mpaka Babeli. 8 Hata mwezi wa tano, siku ya saba ya mwezi, ndio mwaka wa kumi na kenda wa mfalme Nebukadreza, mfalme wa Babeli, Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, mtumishi wa mfalme wa Babeli, akaingia Yerusalemu. 9 Akaiteketeza nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme; na nyumba zote za Yerusalemu, naam, kila nyumba kubwa aliiteketeza kwa moto. 10 Na jeshi lote la Wakaldayo, waliokuwa pamoja na huyo amiri wa askari walinzi, wakazibomoa kuta za Yerusalemu pande zote. 11 Na mabaki ya watu waliosalia katika mji, nao wale walioasi, na kumkimbilia mfalme wa Babeli, na mabaki ya watu wote wengine, watu hao Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawachukua mateka. 12 Lakini huyo amiri wa askari walinzi akawaacha watu walio maskini ili wawe watunza mizabibu na wakulima. 13 Na zile nguzo za shaba zilizokuwako nyumbani mwa Bwana, na matako, na ile bahari ya shaba, iliyokuwamo nyumbani mwa Bwana, Wakaldayo wakavivunja vipande vipande, wakaichukua shaba yake yote mpaka Babeli. 14 Nayo masufuria, na majembe, na makasi, na miiko, na vyombo vyote vya shaba walivyokuwa wakivitumia, wakavichukua vyote. 15 Na vyetezo, na mabakuli; vilivyokuwa vya dhahabu katika dhahabu, na vilivyokuwa vya fedha katika fedha, amiri wa askari walinzi akavichukua. 16 Zile nguzo mbili, na ile bahari moja, na yale matako, Sulemani alivyoifanyia nyumba ya Bwana; shaba ya vyombo hivyo vyote haikuwa na uzani. 17 Urefu wa nguzo moja ulikuwa dhiraa kumi na nane, na kichwa cha shaba kilikuwa juu yake; na urefu wa kichwa ulikuwa dhiraa tatu; na mapambo ya wavu na makomamanga juu ya kichwa hicho kote kote, yote yalikuwa ya shaba. Nayo nguzo ya pili ilikuwa vivyo hivyo, pamoja na ule wavu. 18 Na amiri wa askari walinzi akamtwaa Seraya, kuhani mkuu, na Sefania, kuhani wa pili, na wale walinzi watu wa mlango; 19 na katika mji akamtwaa towashi mmoja, aliyewasimamia watu wa vita; na watu watano katika wale waliosimama mbele ya mfalme, walioonekana mjini; na katibu wa jemadari wa jeshi, aliyewaandika watu wa nchi; na watu sitini katika watu wa nchi, walioonekana mjini. 20 Kisha Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawatwaa hao, akawaleta kwa mfalme wa Babeli huko Ribla. 21 Naye mfalme wa Babeli akawapiga, na kuwaua huko Ribla katika nchi ya Hamathi. Hivyo Yuda wakachukuliwa utumwani kutoka nchi yao. 22 Na kwa habari ya watu waliosalia katika nchi ya Yuda, aliowasaza Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akamweka Gedalia mwana wa Ahikamu mwana wa Shafani awe liwali juu yao. 23 Kisha, wakuu wote wa majeshi, wao na watu wao, waliposikia kwamba mfalme wa Babeli amemweka Gedalia kuwa liwali, wakamwendea Gedalia huko Mispa; nao ni hawa, Ishmaeli mwana wa Nethania, na Yohana mwana wa Karea, na Seraya mwana wa Tanhumethi Mnetofa, na Yezania mwana wa Mmaaka, wao na watu wao. 24 Na Gedalia akawaapia wao na watu wao, akawaambia, Msiogope kwa ajili ya watumishi wa Wakaldayo; kaeni katika nchi; mkamtumikie mfalme wa Babeli; itakuwa vyema kwenu. 25 Lakini ikawa katika mwezi wa saba Ishmaeli mwana wa Nethania, mwana wa Elishama, mmoja wa wazao wa kifalme, na watu kumi pamoja naye, wakamwendea Gedalia, wakampiga hata akafa, na hao Wayahudi na Wakaldayo waliokuwa pamoja naye huko Mispa. 26 Wakaondoka watu wote, wadogo kwa wakubwa, pamoja na wakuu wa majeshi, wakainuka kwenda Misri; kwa kuwa waliwaogopa Wakaldayo. 27 Ikawa katika mwaka wa thelathini na saba wa kuhamishwa kwake Yekonia mfalme wa Yuda ,katika mwezi wa kumi na mbili ,siku ya ishirini na saba ya mwezi ,Evil-merodaki,mfalme wa Babeli ,katika mwaka wa kwanza wa kutawala kwake,akamwinua kichwa Yekonia,mfalme wa Yuda,akamtoa gerezani. 28 Akasema naye maneno mazuri, akaweka kiti chake cha enzi juu ya viti vya enzi vya wafalme waliokuwa pamoja naye huko Babeli; 29 naye akambadilishia mavazi yake ya gerezani, akala chakula mbele yake daima, siku zote za maisha yake. 30 Na kwa posho yake, alipewa posho ya daima na mfalme, siku kwa siku sehemu, siku zote za maisha yake.

1 Mambo ya Nyakati 1

1 Adamu, na Sethi, na Enoshi; 2 na Kenani, na Mahalaleli, na Yaredi; 3 na Henoko, na Methusela, na Lameki; 4 na Nuhu, na Shemu, na Hamu, na Yafethi. 5 Wana wa Yafethi; Gomeri, na Magogu, na Madai, na Yavani, na Tubali, na Mesheki, na Tirasi. 6 Na wana wa Gomeri; Ashkenazi, na Rifathi, na Togama. 7 Na wana wa Yavani; Elisha, na Tarshishi, na Kitimu, na Warodani. 8 Wana wa Hamu; Kushi, na Misri, na Putu, na Kanaani. 9 Na wana wa Kushi; Seba, na Havila, na Sabta, na Raama, na Sabteka. Na wana wa Raama; Sheba, na Dedani. 10 Kushi naye akamzaa Nimrodi; yeye akaanza kuwa mtu hodari katika nchi. 11 Na Misri akazaa Waludi, na Waanami, na Walehabi, na Wanaftuhi, 12 na Wapathrusi, na Wakasluhi; huko ndiko walikotoka Wafilisti, na Wakaftori. 13 Na Kanaani akamzaa Sidoni, mwanawe wa kwanza, na Hethi; 14 na Myebusi, na Mwamori, na Mgirgashi; 15 na Mhivi, na Mwarki, na Msini; 16 na Mwarvadi, na Msemari, na Mhamathi. 17 Wana wa Shemu; Elamu, na Ashuru, na Arfaksadi, na Ludi, na Aramu, na Usi, na Huli, na Getheri, na Mashi. 18 Na Arfaksadi akamzaa Sala, na Sala akamzaa Eberi. 19 Na Eberi akazaliwa wana wawili wa kiume; jina la wa kwanza aliitwa Pelegi, maana katika siku zake nchi iligawanyika; na jina la nduguye aliitwa Yoktani. 20 Na Yoktani akamzaa Almodadi, na Shelefu, na Hasarmawethi, na Yera; 21 na Hadoramu, na Uzali, na Dikla; 22 na Obali, na Abimaeli, na Sheba; 23 na Ofiri, na Havila, na Yobabu. Hao wote ndio wana wa Yoktani. 24 Shemu, na Arfaksadi, na Sala; 25 na Eberi, na Pelegi, na Reu; 26 na Serugi, na Nahori, na Tera; 27 na Abramu, naye ndiye Ibrahimu. 28 Wana wa Ibrahimu; Isaka, na Ishmaeli. 29 Hivi ndivyo vizazi vyao; mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, Nebayothi; kisha Kedari, na Abdeeli, na Mibsamu; 30 na Mishma, na Duma, na Masa, na Hadadi, na Tema; 31 na Yeturi, na, Nafishi, na Kedema. Hao ndio wana wa Ishmaeli. 32 Na wana wa Ketura, suria yake Ibrahimu; yeye akamzaa Zimrani, na Yokshani, na Medani, na Midiani, na Ishbaki, na Shua. Na wana wa Yokshani; Sheba na Dedani. 33 Na wana wa Midiani; Efa, na Eferi, na Hanoki, na Abida, na Eldaa. Hao wote ndio wana wa Ketura. 34 Na Ibrahimu naye akamzaa Isaka. Wana wa Isaka; Esau, na Israeli. 35 Wana wa Esau; Elifazi, na Reueli, na Yeushi, na Yalamu, na Kora. 36 Wana wa Elifazi; Temani, na Omari, na Sefo, na Gatamu, na Kenazi, na, kwa Timna, Amaleki. 37 Wana wa Reueli; Nahathi, na Zera, na Shama, na Miza. 38 Na wana wa Seiri; Lotani, na Shobali, na Sibeoni, na Ana, na Dishoni, na Eseri, na Dishani. 39 Na wana wa Lotani; Hori, na Hemamu; na Timna ni umbu lake Lotani. 40 Wana wa Shobali; Alvani, na Manahathi, na Ebali, na Shefo, na Onamu. Na wana wa Sibeoni; Aya, na Ana. 41 Wana wa Ana; Dishoni. Na wana wa Dishoni; Hemdani, na Eshbani, na Ithrani, na Kerani. 42 Wana wa Eseri; Bilhani, na Zaawani, na Akani. Wana wa Dishani; Usi, na Arani. 43 Basi hawa ndio wafalme waliomiliki katika nchi ya Edomu, kabla hajamiliki mfalme awaye yote juu ya wana wa Israeli; Bela, mwana wa Beori; na jina la mji wake ni Dinhaba. 44 Bela akafa, naye Yobabu, mwana wa Zera, wa Bosra, akamiliki badala yake. 45 Yobabu akafa, naye Hushamu, wa nchi ya Watemani, akamiliki badala yake. 46 Hushamu akafa, naye Hadadi, mwana wa Bedadi, akamiliki badala yake, ambaye aliwapiga Midiani katika uwanja wa Moabu; na jina la mji wake ni Avithi. 47 Hadadi akafa, naye Samla, wa Masreka, akamiliki badala yake. 48 Samla akafa, naye Shauli, wa Rehobothi karibu na Mto, akamiliki badala yake. 49 Shauli akafa, naye Baal-Hanani, mwana wa Akbori, akamiliki badala yake. 50 Baal-Hanani akafa, naye Hadadi akamiliki badala yake; na jina la mji wake ni Pau; na jina la mkewe ni Mehetabeli, binti Matredi, binti Mezahabu. 51 Akafa Hadadi. Na hawa ndio majumbe wa Edomu; jumbe Timna, na jumbe Alva, na jumbe Yethethi; 52 na jumbe Oholibama, na jumbe Ela, na jumbe Pinoni; 53 na jumbe Kenazi, na jumbe Temani, na jumbe Mibsari; 54 na jumbe Magdieli, na jumbe Iramu. Hao ndio majumbe wa Edomu.

1 Mambo ya Nyakati 2

1 Hawa ndio wana wa Israeli; Reubeni, na Simeoni, na Lawi, na Yuda, na Isakari, na Zabuloni; 2 na Dani, na Yusufu, na Benyamini, na Naftali, na Gadi, na Asheri. 3 Wana wa Yuda; Eri, na Onani, na Shela; ambao hao watatu alizaliwa na binti Shua, Mkanaani. Naye Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mbaya machoni pa Bwana; naye akamwua. 4 Na Tamari, mkwewe, akamzalia Peresi, na Zera. Wana wote wa Yuda ni watano. 5 Wana wa Peresi; Hesroni, na Hamuli. 6 Na wana wa Zera; Zabdi, na Ethani, na Hemani, na Kalkoli, na Darda; hao wote ni watano. 7 Na wana wa Karmi; Akani, yule mwenye kutaabisha Israeli, aliyekosa katika kitu kilichowekwa wakfu. 8 Na wana wa Ethani; Azaria. 9 Tena wana wa Hesroni aliozaliwa; Yerameeli, na Ramu, na Kalebu. 10 Na Ramu akamzaa Aminadabu; na Aminadabu akamzaa Nashoni, mkuu wa wana wa Yuda; 11 na Nashoni akamzaa Salmoni; na Salmoni akamzaa Boazi; 12 na Boazi akamzaa Obedi; na Obedi akamzaa Yese; 13 na Yese akamzaa Eliabu, mzaliwa wake wa kwanza, na wa pili Abinadabu, na wa tatu Shama; 14 na wa nne Nethaneli, na wa tano Radai; 15 na wa sita Ozemu, na wa saba Daudi; 16 na maumbu yao ni Seruya, na Abigaili. Na wana wa Seruya walikuwa, Abishai, na Yoabu, na Asaheli; hao watatu. 17 Na Abigaili akamzaa Amasa; na babaye Amasa ni Yetheri, Mwishmaeli. 18 Basi Kalebu, mwana wa Hesroni, akazaliwa wana na mkewe Azubu, na Yeriothi, na hawa ndio wanawe wa kiume; Yesheri, na Shobabu, na Ardoni. 19 Akafa Azuba, naye Kalebu akamtwaa Efrathi, aliyemzalia Huri. 20 Naye Huri akamzaa Uri; na Uri akamzaa Besaleli. 21 Na baadaye Hesroni akamwingilia binti wa Makiri, babaye Gileadi; ambaye alimtwaa alipokuwa mwenye miaka sitini; naye akamzalia Segubu. 22 Na Segubu akamzaa Yairi, aliyekuwa mwenye miji ishirini na mitatu katika nchi ya Gileadi. 23 Na Geshuri na Aramu wakawapokonya miji ya Yairi, pamoja na Kenathi na miji yake, jumla yote miji sitini. Hao wote ni wana wa Makiri, babaye Gileadi. 24 Tena, baada ya kufa kwake Hesroni huko Kalebu-Efrata, ndipo Abia, mkewe Hesroni, alipomzalia Ashuri, babaye Teboa. 25 Na wana wa Yerameeli, mzaliwa wa kwanza wa Hesroni, walikuwa Ramu, mzaliwa wa kwanza, na Buna, na Oreni, na Ozemu; kwa Ahiya. 26 Naye Yerameeli alikuwa na mke mwingine, jina lake Atara; yeye alikuwa mamaye Onamu. 27 Na wana wa Ramu, mzaliwa wa kwanza wa Yerameeli, walikuwa Maasi, na Yamini, na Ekeri. 28 Na wana wa Onamu walikuwa Shamai, na Yada; na wana wa Shamai; Nadabu, na Abishuri. 29 Na mkewe Abishuri aliitwa jina lake Abihaili; naye akamzalia Abani, na Molidi. 30 Na wana wa Nadabu; Seledi, na Apaimu; walakini Seledi alikufa hana watoto. 31 Na wana wa Apaimu; Ishi. Na wana wa Ishi; Sheshani. Na wana wa Sheshani; Alai. 32 Na wana wa Yada, nduguye Shamai; Yetheri, na Yonathani; naye Yetheri akafa hana watoto. 33 Na wana wa Yonathani; Pelethi, na Zaza. Hao ndio wana wa Yerameeli. 34 Basi huyo Sheshani alikuwa hana wana wa kiume, ila binti. Naye Sheshani alikuwa na mtumwa, Mmisri, jina lake akiitwa Yarha. 35 Basi akamwoza binti yake aolewe na Yarha, mtumwa wake; naye akamzalia Atai. 36 Na Atai akamzaa Nathani; na Nathani akamzaa Zabadi; 37 na Zabadi akamzaa Eflali; na Eflali akamzaa Obedi; 38 na Obedi akamzaa Yehu; na Yehu akamzaa Azaria; 39 na Azaria akamzaa Helesi; na Helesi akamzaa Eleasa 40 na Eleasa akamzaa Sismai; na Sismai akamzaa Shalumu; 41 na Shalumu akamzaa Yekamia; na Yekamia akamzaa Elishama. 42 Na wana wa Kalebu, nduguye Yerameeli, walikuwa Mesha, mzaliwa wake wa kwanza, aliyekuwa babaye Zifu; na wana wa Maresha, babaye Hebroni. 43 Na wana wa Hebroni; Kora, na Tapua, na Rekemu, na Shema. 44 Naye Shema akamzaa Rahamu, babaye Yorkeamu; na Rekemu akamzaa Shamai. 45 Na mwana wake Shamai alikuwa Maoni; na Maoni alikuwa babaye Bethsuri. 46 Naye Efa, suria yake Kalebu, alimzaa Harani, na Mosa, na Gazezi; naye Harani akamzaa Gazezi. 47 Na wana wa Yadai; Regemu, na Yothamu, na Geshani, na Peleti, na Efa, na Shaafu. 48 Naye Maaka, suria yake Kalebu, akamzalia Sheberi, na Tirhana. 49 Tena akamzaa Shaafu, babaye Madmana; na Sheva babaye Makbena; na babaye Gibea; naye binti Kalebu alikuwa Aksa. 50 Hao walikuwa wana wa Kalebu. Wana wa Huri, mzaliwa wa kwanza wa Efrathi; Shobali, babaye Kiriath-Yearimu; 51 Salma, babaye Bethlehemu; na Harefu, babaye Beth-gaderi. 52 Naye Shobali, babaye Kiriath-Yearimu, alikuwa na wana; Haroe, na nusu ya Wamenuhothi. 53 Na jamaa za Kiriath-Yearimu; Waithri, na Waputhi, na Washumathi, na Wamishrai; katika hao walitoka Wasorathi, na Waeshtaoli. 54 Na wana wa Salma; Bethlehemu, na Wanetofathi, Atroth-beth-Yoabu, na nusu ya Wamenuhothi, na Wazori. 55 Na jamaa za waandishi waliokaa Yabesi; Watirathi, na Washimeathi, na Wasukathi. Hao ndio Wakeni, waliotoka kwake Hamathi, babaye mbari ya Rekabu.

1 Mambo ya Nyakati 3

1 Basi hawa ndio wana wa Daudi, aliozaliwa huko Hebroni; Amnoni, mzaliwa wa kwanza, mwana wa Ahinoamu, Myezreeli; wa pili, Danieli, wa Abigaili, Mkarmeli; 2 wa tatu, Absalomu, mwana wa Maaka, binti Talmai, mfalme wa Geshuri; wa nne, Adoniya, mwana wa Hagithi; 3 wa tano, Shefatia, wa Abitali; wa sita, Ithreamu, kwa Egla, mkewe. 4 Sita alizaliwa huko Hebroni; na huko akamiliki miaka saba na miezi sita; na huko Yerusalemu akamiliki miaka thelathini na mitatu. 5 Na hawa alizaliwa huko Yerusalemu; Shamua, na Shobabu, na Nathani, na Sulemani, wanne, wana wa Bathsheba, binti Eliamu; 6na Ibhari, na Elishua, na Elipeleti; 7na Noga, na Nefegi, na Yafia; 8 na Elishama, na Eliada, na Elifeleti, watu kenda. 9 Hao wote walikuwa wana wa Daudi, mbali na wana wa masuria; na Tamari alikuwa umbu lao. 10 Na mwanawe Sulemani alikuwa Rehoboamu; na mwanawe huyo alikuwa Abiya; na mwanawe huyo ni Asa; na mwanawe huyo ni Yehoshafati; 11 na mwanawe huyo ni Yehoramu; na mwanawe huyo ni Ahazia; na mwanawe huyo ni Yoashi; 12na mwanawe huyo ni Amazia; na mwanawe huyo ni Uzia; na mwanawe huyo ni Yothamu; 13 na mwanawe huyo ni Ahazi; na mwanawe huyo ni Hezekia; na mwanawe huyo ni Manase; 14na mwanawe huyo ni Amoni; na mwanawe huyo ni Yosia. 15 Na wana wa Yosia walikuwa hawa; Yohana mzaliwa wa kwanza, wa pili Yehoyakimu, wa tatu Sedekia, wa nne Shalumu. 16Na wana wa Yehoyakimu ni hawa; mwanawe Yekonia, na mwanawe Sedekia. 17 Na wana wa Yekonia, huyo aliyechukuliwa mateka; mwanawe Shealtieli, 18na Malkiramu, na Pedaya, na Shenazari, na Yekamia, na Hoshama, na Nedabia. 19 Na wana wa Pedaya; Zerubabeli, na Shimei; na wana wa Zerubabeli; Meshulamu na Hanania; na Shelomithi alikuwa umbu lao; 20 na Hashuba, na Oheli, na Berekia, na Hasadia, na Yushab-Hesedi, watu watano. 21 Na wana wa Hanania; Pelatia na Yeshaya; na wana wa Refaya, na wana wa Arnani, na wana wa Obadia, na wana wa Shekania. 22 Na wana wa Shekania ni hawa; Shemaya, na wana wa Shemaya; Hatushi, na Igali, na Baria, na Nearia, na Shafati, watu sita. 23 Na wana wa Nearia; Elioenai, na Hezekia, na Azrikamu, watu watatu. 24 Na wana wa Elioenai; Hodavia, na Eliashibu, na Pelaya, na Akubu, na Yohana, na Delaya, na Anani, watu saba.

1 Mambo ya Nyakati 4

1 Wana wa Yuda; Peresi, na Hesroni, na Karmi, na Huri, na Shobali. 2 Na Reaya, mwana wa Shobali, akamzaa Yahathi; na Yahathi akawazaa Ahumai, na Lahadi. Hizo ndizo jamaa za Wasorathi. 3 Na hawa ndio wana wa babaye Etamu; Yezreeli, na Ishma, na Idbashi; na umbu lao aliitwa jina lake Haselelponi; 4 na Penueli, babaye Gedori, na Ezeri, babaye Husha. Hao ndio wana wa Huri, mzaliwa wa kwanza wa Efrathi, babaye Bethlehemu. 5 Naye Ashuri, babaye Tekoa, alikuwa na wake wawili, Hela na Naara. 6 Naye Naara akamzalia Ahuzamu, na Heferi, na Temeni, na Ahashtari. Hao ndio wana wa Naara. 7 Na wana wa Hela walikuwa Serethi, na Ishari, na Ethnani. 8 Na Hakosi akawazaa Anubu, na Sobeba, na jamaa za Aharheli, mwana wa Harumu. 9 Naye Yabesi alikuwa mwenye heshima kuliko nduguze; na mamaye akamwita jina lake Yabesi, akisema, Ni kwa sababu nalimzaa kwa huzuni. 10 Huyo Yabesi akamlingana Mungu wa Israeli, akisema, Lau kwamba ungenibarikia kweli kweli, na kunizidishia hozi yangu, na mkono wako ungekuwa pamoja nami, nawe ungenilinda na uovu, ili usiwe kwa huzuni yangu! Naye Mungu akamjalia hayo aliyoyaomba. 11 Naye Kelubu, nduguye Shuha, akamzaa Mehiri, aliyekuwa babaye Eshtoni. 12 Na Eshtoni akamzaa Beth-Rafa, na Pasea, na Tehina, babaye Ir-nahashi. Hao ni watu wa Reka. 13 Na wana wa Kenazi; Othnieli, na Seraya; na wana wa Othnieli; Hathathi. 14 Na Meonothai akamzaa Ofra; na Seraya akamzaa Yoabu, babaye bonde la Wakarashi; kwani hao walikuwa mafundi. 15 Na wana wa Kalebu, mwana wa Yefune; Iru, na Ela, na Naamu; na wana wa Ela; na Kenazi. 16 Na wana wa Yehaleleli; Zifu, na Zifa, na Tiria, na Asareli. 17 Na wana wa Ezrahi; Yetheri, na Meredi, na Eferi, na Yaloni; na Miriamu akamzalia na Shamai, na Ishba, babaye Eshtemoa. 18 Na mkewe Myahudi akawazaa Yeredi, babaye Gedori, na Heberi, babaye Soko, na Yekuthieli, babaye Zanoa. Na hawa ndio wana wa Bithia, binti Farao, ambaye Meredi alimwoa. 19 Na wana wa mkewe Hodia, umbu lake Nahamu, walikuwa babaye Keila, Mgarmi, na Eshtemoa, Mmaaka. 20 Na wana wa Shimoni; Amnoni, na Rina, na Ben-hanani, na Tiloni. Na wana wa Ishi; Zohethi, na Ben-zohethi. 21 Wana wa Shela, mwana wa Yuda; Eri, babaye Leka, na Laada, babaye Maresha, na jamaa zao wa mbari ya wafuma nguo za kitani safi, wa mbari ya Ashbea; 22 na Yokimu, na watu wa Kozeba, na Yoashi, na Sarafi waliokuwa na mamlaka katika Moabu, na Yashubi-lehemu. Na taarifa hizi ni za zamani sana. 23 Hao ndio waliokuwa wafinyanzi, na wenyeji wa Netaimu na Gedera; ndipo walipokaa pamoja na mfalme ili kufanya kazi yake. 24 Wana wa Simeoni; Yemueli, na Yamini, na Yakini, na Sohari, na Shauli; 25 na mwanawe huyo ni Shalumu, na mwanawe huyo ni Mibsamu, na mwanawe huyo ni Mishma. 26 Na wana wa Mishma; mwanawe huyo ni Hamueli, na mwanawe huyo ni Zakuri, na mwanawe huyo ni Shimei. 27 Naye Shimei alikuwa na wana wa kiume kumi na sita, na wana wa kike sita; walakini nduguze walikuwa hawana watoto wengi, tena jamaa yao yote haikuongezeka sana kwa mfano wa wana wa Yuda. 28 Nao wakakaa huko Beer-sheba, na Molada, na Hasar-shuali; 29 na huko Bilha, na Esemu, na Toladi; 30 na huko Bethueli, na Horma, na Siklagi; 31 na huko, Beth-markabothi, na Hasar-susimu, na Bethbiri, na Shaaraimu. Hiyo ndiyo miji yao hata wakati wa kumiliki Daudi. 32 Na vijiji vyao vilikuwa Etamu, na Aini, na Rimoni, na Tokeni, na Ashani, miji mitano, 33 na vijiji vyao vyote vilivyoizunguka miji iyo hiyo, mpaka Baali. Hayo ndiyo makao yao, na hati ya nasaba yao wanayo. 34 Naye Meshobabu, na Yamleki, na Yosha, mwana wa Amazia; 35 na Yoeli, na Yehu, mwana wa Yoshibia, mwana wa Seraya, mwana wa Asieli; 36 na Elioenai, na Yaakoba, na Yeshohava, na Asaya, na Adieli, na Yesimieli, na Benaya; 37 na Ziza, mwana wa Shifi, mwana wa Aloni, mwana wa Yedaya mwana wa Shimri, mwana wa Shemaya; 38 hao waliotajwa majina yao ndio waliokuwa wakuu katika jamaa zao; na mbari za baba zao zikaongezeka sana. 39 Basi wakaenda mpaka maingilio ya Gedori, naam, mpaka upande wa mashariki wa bonde hilo, ili kuwatafutia kondoo zao malisho. 40 Wakaona malisho ya unono, mazuri, na nchi yenyewe ilikuwa na nafasi, tena imetulia, na kuwa na amani; kwani waliokaa huko zamani walikuwa watu wa Hamu. 41 Na hao walioandikwa majina yao waliingia huko katika siku za Hezekia, mfalme wa Yuda, na kuzipiga hema zao, pamoja na hao Wameuni walioonekana huko, wakawaangamiza kabisa, hata siku hii ya leo, nao wakakaa huko badala yao; kwa sababu huko kulikuwa na malisho kwa kondoo zao. 42 Na baadhi yao, maana ya hao wana wa Simeoni, watu mia tano, wakaenda mpaka mlima Seiri, na majemadari wao walikuwa Pelatia, na Nearia, na Refaya, na Uzieli, wana wa Ishi. 43 Nao wakawapiga mabaki ya Waamaleki waliookoka, wakakaa huko, hata siku hii ya leo.

1 Mambo ya Nyakati 5

1 Na wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli; (kwa maana ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza, lakini, kwa kuwa alikinajisi kitanda cha babaye, haki yake ya mzaliwa wa kwanza walipewa wana wa Yusufu, mwana wa Israeli; tena nasaba isihesabiwe kwa kuifuata hiyo haki ya mzaliwa wa kwanza. 2 Kwani Yuda ndiye aliyeshinda miongoni mwa nduguze, na kwake ndiko alikotoka mtawala; bali haki ile ya mzaliwa wa kwanza alipewa Yusufu); 3 wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli; Hanoki, na Palu, na Hesroni, na Karmi. 4 Wana wa Yoeli; mwanawe huyo ni Shemaya, na mwanawe huyo ni Gogu, na mwanawe huyo ni Shimei; 5 na mwanawe huyo ni Mika, na mwanawe huyo ni Reaya, na mwanawe huyo ni Baali; 6 na mwanawe huyo ni Beera, ambaye Tiglath-Pileseri, mfalme wa Ashuru, alimchukua mateka; ndiye aliyekuwa mkuu wa Wareubeni. 7 Na nduguze kwa jamaa zao, hapo ilipohesabiwa nasaba ya vizazi vyao; mkuu wao, Yeieli, na Zekaria, 8 na Bela, mwana wa Azazi, mwana wa Shemaya, mwana wa Yoeli, aliyekaa huko Aroeri, hata kufika Nebo na Baal-meoni; 9 na upande wa mashariki akakaa hata kufika maingilio ya jangwa litokalo mto wa Frati; kwa sababu ng'ombe zao walikuwa wameongezeka sana katika nchi ya Gileadi. 10 Na katika siku za Sauli wakapigana vita na Wahajiri, ambao waliangushwa kwa mikono yao; nao wakakaa katika hema zao katika nchi yote upande wa mashariki wa Gileadi. 11 Na wana wa Gadi walikuwa wakikaa kwa kuwaelekea, katika nchi ya Bashani mpaka Saleka; 12 Yoeli, alikuwa mkuu wao, na wa pili Shafamu, na Yanai, na Shafati, katika Bashani; 13 na ndugu zao wa mbari za baba zao; Mikaeli, na Meshulamu, na Sheba, na Yorai, na Yakani, na Zia, na Eberi, watu saba. 14 Hao ndio wana wa Abihaili, mwana wa Huri, mwana wa Yaroa, mwana wa Gileadi, mwana wa Mikaeli, mwana wa Yehishai, mwana wa Yado, mwana wa Buzi; 15 Ahi, mwana wa Abdieli, mwana wa Guni, alikuwa mkuu wa mbari za baba zao. 16 Nao wakakaa huko Gileadi, katika Bashani, na katika miji yake, na katika viunga vyote vya Sharoni, hata kufika mipakani mwake. 17 Hao wote walihesabiwa kwa nasaba, katika siku za Yothamu, mfalme wa Yuda, na siku za Yeroboamu, mfalme wa Israeli. 18 Wana wa Reubeni, na Wagadi, na nusu-kabila ya Manase, watu mashujaa, wawezao kuchukua ngao na upanga, na kupiga upinde, wenye ustadi katika kupigana vita, walikuwa watu arobaini na nne elfu mia saba na sitini, walioweza kwenda vitani. 19 Nao wakapigana vita na Wahajiri; na Yeturi, na Nafishi, na Nodabu. 20Wakapata msaada juu yao, nao Wahajiri walitiwa mikononi mwao, na wote waliokuwa pamoja nao; kwa kuwa walimlingana Mungu pale vitani; naye akayatakabali maombi yao, kwa sababu walimtumaini yeye. 21 Wakateka nyara ng'ombe zao, na ngamia zao hamsini elfu, na kondoo zao mia mbili na hamsini elfu, na punda zao elfu mbili; na watu mia elfu. 22 Kwani wengi walianguka waliouawa, kwa sababu vita vile vilikuwa vya Mungu. Nao wakakaa badala yao hata wakati wa ule uhamisho. 23 Na wana wa nusu-kabila ya Manase walikaa katika nchi; nao wakaongezeka kutoka Bashani mpaka Baal-hermoni, na Seniri, na mlima Hermoni. 24 Na hawa ndio wakuu wa mbari za baba zao; Eferi, na Ishi, na Elieli, na Azrieli, na Yeremia, na Hodavia, na Yadieli; watu hodari wa vita, watu mashuhuri, wakuu wa mbari za baba zao. 25 Nao wakamwasi Mungu wa baba zao, wakaenda kufanya uasherati na miungu ya watu wa nchi, ambao Mungu alikuwa amewaangamiza mbele yao. 26 Naye Mungu wa Israeli akamwamsha roho Pulu, mfalme wa Ashuru na roho ya Tiglath-Pileseri, mfalme wa Ashuru, naye akawachukua mateka hao Wareubeni, na Wagadi, na nusu-kabila ya Wamanase; akawaleta mpaka Hala, na Habori, na Hara, na mpaka mto wa Gozani, hata siku hii ya leo.

1 Mambo ya Nyakati 6

1 Wana wa Lawi; Gershoni, na Kohathi, na Merari. 2 Na wana wa Kohathi; Amramu, na Ishari, na Hebroni, na Uzieli. 3 Na wana wa Amramu; Haruni, na Musa, na Miriamu. Na wana wa Haruni; Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari. 4 Eleazari akamzaa Finehasi; na Finehasi akamzaa Abishua; 5 na Abishua akamzaa Buki; na Buki akamzaa Uzi; 6 na Uzi akamzaa Zerahia; na Zerahia akamzaa Merayothi, 7 na Merayothi akamzaa Amaria; na Amaria akamzaa Ahitubu; 8 na Ahitubu akamzaa Sadoki; na Sadoki akamzaa Ahimaasi; 9 na Ahimaasi akamzaa Azaria; na Azaria akamzaa Yohana; 10 na Yohana akamzaa Azaria (ndiye huyo aliyefanya kazi ya ukuhani katika nyumba aliyoijenga Sulemani huko Yerusalemu) 11 na Azaria akamzaa Amaria; na Amaria akamzaa Ahitubu; 12 na Ahitubu akamzaa Sadoki; na Sadoki akamzaa Meshulamu; 13 na Meshulamu akamzaa Hilkia; na Hilkia akamzaa Azaria; 14 na Azaria akamzaa Seraya; na Seraya akamzaa Yehosadaki; 15 na Yehosadaki akachukuliwa mateka, hapo Bwana alipowachukua mateka Yuda na Yerusalemu, kwa mkono wa Nebukadreza. 16 Wana wa Lawi; Gershoni, na Kohathi, na Merari. 17 Na haya ndiyo majina ya wana wa Gershoni; Libni, na Shimei. 18 Na wana wa Kohathi walikuwa Amramu, na Ishari, na Hebroni, na Uzieli. 19 Wana wa Merari; Mali, na Mushi. Na hizi ndizo jamaa za Walawi, sawasawa na mbari za baba zao. 20 Wa Gershoni; mwanawe huyo ni Libni, na mwanawe huyo ni Yahathi, na mwanawe huyo ni Zima; 21 na mwanawe huyo ni Yoa, na mwanawe huyo ni Ido, na mwanawe huyo ni Zera, na mwanawe huyo ni Yeatherai. 22 Wana wa Kohathi; mwanawe huyo ni Ishari, na mwanawe huyo ni Kora, na mwanawe huyo ni Asiri; 23 na mwanawe huyo ni Elkana, na mwanawe huyo ni Ebiasafu, na mwanawe huyo ni Asiri; 24 na mwanawe huyo ni Tahathi, na mwanawe huyo ni Urieli, na mwanawe huyo ni Uzia, na mwanawe huyo ni Shauli. 25 Na wana wa Elkana; Amasai, na Ahimothi. 26 Kwa habari za Elkana; wana wa Elkana; mwanawe huyo ni Sufu, na mwanawe huyo ni Tohu; 27 na mwanawe huyo ni Elihu, na mwanawe huyo ni Yerohamu, na mwanawe huyo ni Elkana. 28 Na wana wa Samweli; Yoeli, mzaliwa wa kwanza, na wa pili Abia. 29 Wana wa Merari; Mali, na mwanawe huyo ni Libni, na mwanawe huyo ni Shimei, na mwanawe huyo ni Uza; 30 na mwanawe huyo ni Shimea, na mwanawe huyo ni Hagla, na mwanawe huyo ni Asaya. 31 Na hawa ndio watu aliowaweka Daudi juu ya kazi ya kuimba katika nyumba ya Bwana, sanduku lile lilipokwisha pata mahali pa kustarehe. 32 Nao wakafanya kazi yao ya kuimba mbele ya maskani ya hema ya kukutania, hata Sulemani alipokuwa amejenga ile nyumba ya Bwana huko Yerusalemu; pia wakaisimamia huduma yao sawasawa na zamu zao. 33 Na hawa ndio waliofanya huduma pamoja na wana wao. Katika wana wa Wakohathi; Hemani mwimbaji, mwana wa Yoeli, mwana wa Samweli; 34 mwana wa Elkana, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu; 35 mwana wa Sufu, mwana wa Elkana, mwana wa Mahathi, mwana wa Amasai; 36 mwana wa Elkana, mwana wa Shauli, mwana wa Uzia, mwana wa Urieli; 37 mwana wa Tahathi, mwana wa Asiri, mwana wa Ebiasafu, mwana wa Kora; 38 mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, mwana wa Israeli. 39 Na nduguye Asafu, aliyesimama upande wake wa kuume, huyo Asafu alikuwa mwana wa Berekia, mwana wa Shimea; 40 mwana wa Mikaeli, mwana wa Baaseya, mwana wa Malkiya; 41 mwana wa Yeatherai, mwana wa Zera, mwana wa Ido; 42 mwana wa Yoa, mwana wa Zima, mwana wa Shimei; 43 mwana wa Yahathi, mwana wa Gershoni, mwana wa Lawi. 44 Na upande wa kushoto ndugu zao, wana wa Merari; Ethani, mwana wa Kishi, mwana wa Abdi, mwana wa Maluki; 45 mwana wa Hashabia, mwana wa Amazia, mwana wa Hilkia; 46 mwana wa Amzi, mwana wa Bani, mwana wa Shemeri; 47 mwana wa Mali, mwana wa Mushi, mwana wa Merari, mwana wa Lawi. 48 Na ndugu zao, Walawi, ndio waliowekwa ili kufanya huduma yote ya maskani ya nyumba ya Mungu. 49 Lakini Haruni na wanawe ndio waliokuwa wakitoa sadaka juu ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, na juu ya madhabahu ya kufukizia uvumba, kwa ajili ya kazi yote ya Patakatifu pa Patakatifu, ili kufanya upatanisho kwa Israeli, sawasawa na yote aliyokuwa ameyaamuru Musa, mtumishi wa Mungu. 50 Na hawa ndio wana wa Haruni; mwanawe huyo ni Eleazari, na mwanawe huyo ni Finehasi, na mwanawe huyo ni Abishua; 51 na mwanawe huyo ni Buki, na mwanawe huyo ni Uzi, na mwanawe huyo ni Serahia; 52 na mwanawe huyo ni Merayothi, na mwanawe huyo ni Amaria, na mwanawe huyo Ahitubu; 53 na mwanawe huyo ni Sadoki, na mwanawe huyo ni Ahimaasi. 54 Basi haya ndiyo makao yao, sawasawa na marago yao mipakani mwao; wana wa Haruni, katika jamaa za Wakohathi; kwani walikuwa na kura ya kwanza; 55 wakapewa Hebroni, katika nchi ya Yuda, na vijiji vyake vilivyouzunguka; 56 bali mashamba ya mji huo, na vijiji vyake, alipewa Kalebu, mwana wa Yefune. 57 Na wana wa Haruni wakapewa miji ile ya kukimbilia, nayo ni Hebroni, tena Libna pamoja na viunga vyake, na Yatiri, na Eshtemoa pamoja na viunga vyake; 58 na Holoni pamoja na viunga vyake, na Debiri pamoja na viunga vyake; 59 na Ashani pamoja na viunga vyake, na Beth-shemeshi pamoja na viunga vyake; 60 tena katika kabila ya Benyamini; Geba pamoja na viunga vyake, na Alemethi pamoja na viunga vyake, na Anathothi pamoja na viunga vyake. Miji yao yote katika jamaa zao ilikuwa miji kumi na mitatu. 61 Nao waliobaki wa wana wa Kohathi walipewa kwa kura miji kumi, katika jamaa ya kabila hiyo, yaani, nusu-kabila, nusu ya Manase. 62 Na wana wa Gershoni walipewa kwa kura miji kumi na mitatu, sawasawa na jamaa zao, katika kabila ya Isakari, na katika kabila ya Asheri, na katika kabila ya Naftali, na katika kabila ya Manase waliokaa Bashani. 63 Na wana wa Merari walipewa kwa kura miji kumi na miwili, sawasawa na jamaa zao, katika kabila ya Reubeni, na katika kabila ya Gadi, na katika kabila ya Zabuloni. 64 Na wana wa Israeli waliwapa Walawi miji hiyo pamoja na viunga vyake. 65 Tena wakawapa kwa kura miji hiyo iliyotajwa majina yake, katika kabila ya wana wa Yuda, na katika kabila ya wana wa Simeoni, na katika kabila ya wana wa Benyamini. 66 Na jamaa nyingine za wana wa Kohathi walikuwa na miji ya mipakani mwao katika kabila ya Efraimu. 67 Basi wakapewa miji ya kukimbilia, yaani, Shekemu pamoja na viunga vyake katika nchi ya milima milima ya Efraimu; na Gezeri pamoja na viunga vyake; 68 na Yokmeamu pamoja na viunga vyake, na Beth-horoni pamoja na viunga vyake; 69 na Aiyaloni pamoja na viunga vyake, na Gath-rimoni pamoja na viunga vyake; 70 na katika nusu-kabila ya Manase; Taanaki pamoja na viunga vyake, na Ibleamu pamoja na viunga vyake; kwa mabaki ya jamaa ya wana wa Kohathi. 71 Na wana wa Gershoni wakapewa, katika jamaa ya nusu-kabila ya Manase; Golani katika Bashani pamoja na viunga vyake, na Ashtarothi pamoja na viunga vyake; 72 na katika kabila ya Isakari; Kishioni pamoja na viunga vyake, na Daberathi pamoja na viunga vyake; 73 na Remethi pamoja na viunga vyake, na En-gaminu pamoja na viunga vyake; 74 na katika kabila ya Asheri; Mishali pamoja na viunga vyake, na Abdoni pamoja na viunga vyake; 75 na Helkathi pamoja na viunga vyake, na Rehobu pamoja na viunga vyake; 76 na katika kabila ya Naftali; Kedeshi katika Galilaya pamoja na viunga vyake, na Hamothi pamoja na viunga vyake, na Kiriathaimu pamoja na viunga vyake. 77 Nao mabaki ya Walawi, wana wa Merari, wakapewa, katika kabila ya Zabuloni; Rimona pamoja na viunga vyake, na Tabori pamoja na viunga vyake; 78 na ng'ambo ya mto wa Yordani huko Yeriko, upande wa mashariki wa Yordani, katika kabila ya Reubeni; Bezeri katika nyika pamoja na viunga vyake, na Yahasa pamoja na viunga vyake, 79 na Kedemothi pamoja na viunga vyake, na Mefaathi pamoja na viunga vyake; 80 na katika kabila ya Gadi; Ramothi katika Gileadi pamoja na viunga vyake, na Mahanaimu pamoja na viunga vyake; 81 na Heshboni pamoja na viunga vyake, na Yazeri pamoja na viunga vyake.

1 Mambo ya Nyakati 7

1 Na wana wa Isakari; Tola, na Puva, na Yashubu, na Shimroni, wanne. 2 Na wana wa Tola; Uzi, na Refaya, na Yerieli, na Yamai, na Ibsamu, na Shemueli, wakuu wa mbari za baba zao, yaani, wa Tola; watu hodari wa vita katika vizazi vyao; hesabu yao katika siku za Daudi ilikuwa watu ishirini na mbili elfu na mia sita. 3 Na wana wa Uzi; Izrahia; na wana wa Izrahia; Mikaeli, na Obadia, na Yoeli, na Ishia, watano; wote wakuu. 4 Na pamoja nao, katika vizazi vyao, sawasawa na mbari za baba zao, walikuwapo vikosi vya jeshi la vita, watu thelathini na sita elfu; kwa kuwa wake zao na watoto wao walikuwa wengi. 5 Na ndugu zao katika jamaa zote za Isakari, watu hodari wa vita, wakihesabiwa kwa vizazi vyao, walikuwa watu themanini na saba elfu. 6 Wana wa Benyamini; Bela, na Bekeri, na Yediaeli, watatu. 7 Na wana wa Bela; Esboni, na Uzi, na Uzieli, na Yerimothi, na Iri, watano; wakuu wa mbari za baba zao, watu hodari wa vita; nao wakahesabiwa kwa vizazi vyao watu ishirini na mbili elfu na thelathini na wanne. 8 Na wana wa Bekeri; Zemira, na Yoashi, na Eliezeri, na Elioenai, na Omri, na Yeremothi, na Abiya, na Anathothi, na Alemethi. Hao wote ndio wana wa Bekeri. 9 Nao wakahesabiwa kwa vizazi vyao, katika vizazi vyao, wakuu wa mbari za baba zao, watu hodari wa vita, jumla yao watu ishirini elfu na mia mbili. 10 Na wana wa Yediaeli; Bilhani; na wana wa Bilhani; Yeushi, na Benyamini, na Ehudi, na Kenaana, na Zethani, na Tarshishi, na Ahishahari. 11 Hao wote ndio wana wa Yediaeli, sawasawa na wakuu wa mbari za baba zao, watu hodari wa vita, kumi na saba elfu na mia mbili, wawezao kwenda vitani katika jeshi. 12 Tena Shupimu, na Hupimu, wana wa Iri; na Hushimu, wana wa Aheri. 13 Wana wa Naftali; Yaseeli, na Guni, na Yeseri, na Shilemu; wana wa Bilha. 14 Wana wa Manase; Asrieli, ambaye suria yake, Mwarami, alimzalia, akamzalia na Makiri babaye Gileadi; 15 naye Makiri akatwaa mke kwa Hupimu na Shupimu, ambao umbu lao aliitwa Maaka; na wa pili akaitwa jina lake Selofehadi; na Selofehadi alikuwa na binti. 16 Na Maaka mkewe Makiri, akamzalia mwana, akamwita jina lake Pereshi; na jina la nduguye aliitwa Shereshi; na wanawe walikuwa Ulamu, na Rakemu. 17 Na wana wa Ulamu; Bedani. Hao ndio wana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase. 18 Na umbu lake, Hamolekethi, akamzaa Ish-hodu, na Abiezeri, na Mala. 19 Na wana wa Shemida walikuwa Ahiani, na Shekemu, na Liki, na Aniamu. 20 Na wana wa Efraimu; Shuthela, na mwanawe huyo ni Beredi, na mwanawe huyo ni Tahathi, na mwanawe huyo ni Ekada, na mwanawe huyo ni Tahathi; 21 na mwanawe huyo ni Zabadi, na mwanawe huyo ni Shuthela; na Ezeri na Ekadi, ambao watu wa Gathi, wenyeji wa nchi, waliwaua, kwa sababu walishuka ili kuzipokonya ng'ombe zao. 22 Na Efraimu, baba yao, akaomboleza siku nyingi, wakaja nduguze ili kumfariji. 23 Naye akamwingilia mkewe, naye akachukua mimba na kuzaa mwana, akamwita jina lake Beria, kwa sababu mna mabaya nyumbani mwake. 24 Na binti yake alikuwa Sheera, ambaye alijenga Beth-horoni, wa chini na wa juu, na Uzen-sheera. 25 Mwanawe ni Refa, na Reshefu, na mwanawe huyo ni Tela, na mwanawe huyo ni Tahani; 26 na mwanawe huyo ni Ladani, na mwanawe huyo ni Amihudi, na mwanawe huyo ni Elishama; 27 na mwanawe huyo ni Nuni, na mwanawe huyo ni Yoshua. 28 Na hizi ndizo hozi zao na makao yao; Betheli na vijiji vyake, na upande wa mashariki Naara, na upande wa magharibi Gezeri na vijiji vyake; na Shekemu pia na vijiji vyake, hata Aza na vijiji vyake; 29 na mipakani mwa wana wa Manase; Beth-sheani na vijiji vyake; na Taanaki na vijiji vyake; na Megido na vijiji vyake; na Dori na vijiji vyake. Katika miji hiyo walikaa wana wa Yusufu, mwana wa Israeli. 30 Wana wa Asheri; Imna, na Ishva, na Ishvi, na Beria, na umbu lao, Sera. 31 Na wana wa Beria; Heberi, na Malkieli, aliyekuwa babaye Birzaithi. 32 Na Heberi akamzaa Yafleti, na Shomeri, na Hothamu, na umbu lao, Shua. 33 Na wana wa Yafleti; Pasaki, na Bimhali, na Ashvathi. Hao ndio wana wa Yafleti. 34 Na wana wa Shomeri; Ahi, na Roga, na Yehuba, na Aramu. 35 Na wana wa nduguye Helemu; Sofa, na Imna, na Sheleshi, na Amali. 36 Wana wa Sofa; Sua, na Harneferi, na Shuali, na Beri, na Imra; 37 na Bezeri, na Hodu, na Shama, na Shilsha, na Ithrani, na Beera. 38 Na wana wa Yetheri; Yefune, na Pispa, na Ara. 39 Na wana wa Ula; Ara, na Hanieli na Risia. 40 Hao wote ndio wana wa Asheri, wakuu wa mbari za baba zao, watu wateule, hodari wa vita, wakuu wa mashehe. Na hesabu yao waliojumlishwa kwa vizazi vyao kwenda vitani walikuwa watu ishirini na sita elfu.

1 Mambo ya Nyakati 8

1 Naye Benyamini akamzaa Bela, mzaliwa wake wa kwanza, na wa pili Ashbeli, na wa tatu Ahiramu; 2 na wa nne Noha, na wa tano Rafa. 3 Na Bela alikuwa na wana; Adari, na Gera, na Abihudi; 4 na Abishua, na Naamani, na Ahoa; 5 na Gera, na Shufamu, na Huramu. 6 Na hawa ndio wana wa Ehudi. (Hao ndio wakuu wa mbari za baba zao miongoni mwa wenyeji wa Geba; nao wakawachukua mateka mpaka Manahathi; 7 na Naamani, na Ahoa, na Gera; aliwachukua mateka). Naye akamzaa Uza, na Ahihudi. 8 Na Shaharaimu akazaa watoto katika Bara-Moabu, baada ya kuwafukuza wakeze Hushimu na Baara. 9 Akazaliwa na Hodeshi, mkewe; Yobabu, na Sibia, na Mesha, na Malkamu; 10 na Yeusi, na Shakia, na Mirma. Hao ndio wanawe, wakuu wa mbari za baba zao. 11 Naye alikuwa amezaliwa na Hushimu, Abitubu, na Elpaali. 12 Na wana wa Elpaali; Eberi, na Mishamu, na Shemedi, ambaye ndiye aliyejenga Ono na Lodi, pamoja na vijiji vyake; 13 na Beria, na Shema, waliokuwa wakuu wa mbari za baba zao miongoni mwa wenyeji wa Aiyaloni, wale ambao waliwakimbiza wenyeji wa Gathi. 14 Na Ahio, na Ghashaki, na Yeremothi; 15 na Zebadia, na Aradi, na Ederi; 16 na Mikaeli, na Ishpa, na Yoha; walikuwa wana wa Beria. 17 Na Zebadia, na Meshulamu, na Hizki, na Heberi; 18 na Ishmerai, na Izlia, na Yobabu; walikuwa wana wa Elpaali. 19 Na Yakimu, na Zikri, na Zabdi; 20 na Elienai, na Silethai, na Elieli; 21 na Adaya, na Beraya, na Shimrathi; walikuwa wana wa Shema. 22 Na Ishpani, na Eberi, na Elieli; 23 na Abdoni, na Zikri, na Hanani; 24 na Hanania, na Elamu, na Anthothiya; 25 na Ifdeya, na Penueli; walikuwa wana wa Shashaki. 26 Na Shamsherai, na Sheharia, na Athalia; 27 na Yaareshia, na Eliya, na Zikri; walikuwa wana wa Yerohamu. 28 Hao ndio waliokuwa wakuu wa mbari za baba zao, katika vizazi vyao vyote, watu maarufu; na hao walikuwa wakikaa Yerusalemu. 29 Basi huko Gibea alikaa babaye Gibea, jina lake Yeieli, ambaye jina la mkewe aliitwa Maaka; 30 na mwanawe, mzaliwa wake wa kwanza, alikuwa Abdoni, na Suri, na Kishi, na Baali, na Nadabu; 31 na Gedori, na Ahio, na Zekaria 32 Na Miklothi akamzaa Shimea. Na hao nao walikuwa wakikaa pamoja na ndugu zao huko Yerusalemu, kuwakabili ndugu zao. 33 Naye Neri akamzaa Kishi; na Kishi akamzaa Sauli; na Sauli akamzaa Yonathani, na Malkishua, na Abinadabu, na Eshbaali. 34 Na mwanawe Yonathani alikuwa Meribaali; na Meribaali akamzaa Mika. 35 Na wana wa Mika; Pithoni, na Meleki, na Tarea, na Ahazi. 36 Na Ahazi akamzaa Yara; na Yara akamzaa Alemethi, na Azmawethi, na Zimri; na Zimri akamzaa Mosa; 37 na Mosa akamzaa Binea; na mwanawe huyo alikuwa Refaya, na mwanawe huyo ni Ekasa, na mwanawe huyo ni Aseli; 38 naye Aseli alikuwa na wana sita, ambao majina yao ni haya; Azrikamu, na Bokeru, na Ishmaeli, na Shearia, na Obadia, na Hanani. Hao wote walikuwa wana wa Aseli. 39 Na wana wa Esheki nduguye ni hawa; mzaliwa wake wa kwanza, Ulamu, na wa pili Yeushi, na wa tatu Elifeleti. 40 Na wana wa Ulamu walikuwa watu hodari wa vita, wapiga upinde, nao walikuwa na wana wengi, na wana wa wana, watu mia na hamsini. Hao wote ndio waliokuwa wana wa Benyamini.

1 Mambo ya Nyakati 9

1 Hivyo Israeli wote walihesabiwa kwa nasaba; na tazama, hizo zimeandikwa katika kitabu cha wafalme wa Israeli; na Yuda wakachukuliwa mateka mpaka Babeli, kwa sababu ya makosa yao. 2 Basi wenyeji wa kwanza waliokaa katika hozi zao katika miji yao walikuwa Israeli, na makuhani, na Walawi, na Wanethini. 3 Na huko Yerusalemu walikuwa wakikaa baadhi ya wana wa Yuda, na wana wa Benyamini, na wana wa Efraimu na Manase; 4 Uthai, mwana wa Amihudi, mwana wa Omri, mwana wa Imli, mwana wa Bani, wa wana wa Peresi, mwana wa Yuda. 5 Na wa Washiloni; Asaya, mzaliwa wa kwanza, na wanawe. 6 Na wa wana wa Zera; Yeueli, na ndugu zao; watu mia sita na tisini. 7 Na wa wana wa Benyamini; Salu, mwana wa Meshulamu, mwana wa Hodavia, mwana wa Hasenua; 8 na Ibneya, mwana wa Yerohamu; na Ela, mwana wa Uzi, mwana wa Mikri; na Meshulamu, mwana wa Shefatia, mwana wa Reueli, mwana wa Ibniya; 9 na ndugu zao, sawasawa na vizazi vyao; watu mia kenda na hamsini na sita. Watu hao wote ndio waliokuwa wakuu wa mbari za baba zao, kwa kadiri ya mbari za baba zao. 10 Na katika makuhani; Yedaya, na Yehoyaribu, na Yakini; 11 na Azaria, mwana wa Hilkia, mwana wa Meshulamu, mwana wa Sadoki, mwana wa Merayothi, mwana wa Ahitubu, mkuu wa nyumba ya Mungu; 12 na Adaya, mwana wa Yerohamu, mwana wa Pashuri, mwana wa Malkiya; na Maasai, mwana wa Adieli, mwana wa Yazera, mwana wa Meshulamu, mwana wa Meshilemithi, mwana wa Imeri; 13 wakuu wa mbari za baba zao; pamoja na ndugu zao; watu elfu na mia saba na sitini; watu wenye ustadi waliofaa sana kwa kazi ya huduma ya nyumba ya Mungu. 14 Na katika Walawi; Shemaya, mwana wa Hashubu, mwana wa Azrikamu, mwana wa Hashabia, wa wana wa Merari; 15 na Bakbakari, na Hereshi, na Galali, na Matania, mwana wa Mika, mwana wa Zikri, mwana wa Asafu; 16 na Obadia, mwana wa Shemaya, mwana wa Galali, mwana wa Yeduthuni; na Berekia, mwana wa Asa, mwana wa Elkana; waliokaa katika vijiji vya Wanetofathi. 17 Na katika mabawabu; Shalumu, na Akubu, na Talmoni, na Ahimani, na ndugu zao; naye Shalumu alikuwa mkuu wao; 18 ambao tangu hapo walikuwa wakingojea penye lango la mfalme upande wa mashariki; hao ndio waliokuwa wangojezi wa rago la wana wa Lawi. 19 Naye Shalumu, mwana wa Kore, mwana wa Ebiasafu, mwana wa Kora; pamoja na nduguze wa mbari ya babaye, Wakora; walikuwa wakiisimamia kazi hiyo ya huduma, wenye ungojezi wa malango ya maskani; na baba zao walikuwa wamesimamia matuo ya Bwana, wakiyalinda maingilio; 20 naye Finehasi, mwana wa Eleazari, alikuwa mkuu wao hapo zamani, naye Bwana alikuwa pamoja naye. 21 Zekaria, mwana wa Meshelemia, alikuwa bawabu mlangoni pa ile hema ya kukutania. 22 Hao wote waliochaguliwa kuwa wangojezi wa malango walikuwa watu mia mbili na kumi na wawili. Nao wakahesabiwa kwa nasaba katika vijiji vyao, ambao Daudi na Samweli, huyo mwonaji, walikuwa wamewaweka katika kazi yao waliyoamaniwa. 23 Basi watu hao na wana wao walikuwa na usimamizi wa malango ya nyumba ya Bwana, yaani, nyumba ya maskani, kwa zamu. 24 Hao wangojezi walikuwapo pande zote nne, kuelekea mashariki, na magharibi, na kaskazini, na kusini. 25 Na ndugu zao, katika vijiji vyao, wakaamaniwa kuingia kila siku ya saba, zamu kwa zamu, ili kuwa pamoja nao; 26 kwa maana wale wangojezi wanne, waliokuwa wakuu, nao ni Walawi, walikuwa na kazi ya kuamaniwa, tena walikuwa juu ya vyumba na juu ya hazina katika nyumba ya Mungu. 27 Nao wakalala kandokando nyumbani mwa Mungu, kwa kuwa ulinzi wake ulikuwa juu yao, nayo ilikuwa kazi yao kuyafungua malango asubuhi baada ya asubuhi. 28 Na baadhi yao walikuwa na ulinzi wa vyombo vya huduma; kwani huingizwa kwa hesabu, na kutolewa kwa hesabu vile vile. 29 Na baadhi yao waliamaniwa kuviangalia vyombo vya nyumbani, na vyombo vyote vya Patakatifu; na kuwa juu ya unga safi, na divai, na mafuta, na ubani, na manukato. 30 Na baadhi ya wana wa makuhani waliweka tayari machanganyiko ya manukato. 31 Naye Matithia, Mlawi mmojawapo, aliyekuwa mzaliwa wa kwanza wa Shalumu, Mkora, aliamaniwa kazi ya kuviangalia vitu vile vilivyookwa kaangoni. 32 Na baadhi ya ndugu zao, wa wana wa Wakohathi, walikuwa juu ya mikate ile ya Wonyesho, ili kuiandaa kila sabato. 33 Tena hawa ndio waimbaji, wakuu wa mbari za baba zao katika Walawi, ambao walikaa vyumbani, kisha walikuwa hawana kazi nyingine; kwa kuwa walitumika katika kazi yao mchana na usiku. 34 Hao walikuwa wakuu wa mbari za baba zao katika Walawi, katika vizazi vyao vyote, watu wakuu; nao walikuwa wakikaa huko Yerusalemu. 35 Basi huko Gibea alikaa babaye Gibea, jina lake Yeieli, na jina la mkewe aliitwa Maaka; 36 na mwanawe, mzaliwa wake wa kwanza, alikuwa Abdoni; na Suri, na Kishi, na Baali, na Meri, na Nadabu; 37 na Gedori, na Ahio, na Zekaria, na Miklothi. 38 Na Miklothi akamzaa Shimea. Hao nao walikuwa wakikaa pamoja na ndugu zao huko Yerusalemu, kuwakabili ndugu zao. 39 Naye Neri akamzaa Kishi; na Kishi akamzaa Sauli; na Sauli akamzaa Yonathani, na Malkishua, na Abinadabu, na Eshbaali. 40 Na mwana wa Yonathani alikuwa Meribaali; na Meribaali akamzaa Mika. 41 Na wana wa Mika; Pithoni, na Meleki, na Tarea. 42 Na Ahazi akamzaa Yara; na Yara akamzaa Alemethi, na Azmawethi, na Zimri; na Zimri akamzaa Mosa; 43 na Mosa akamzaa Binea; na mwanawe huyo alikuwa Refaya, na mwanawe huyo ni Eleasa, na mwanawe huyo ni Aseli; 44 naye Aseli alikuwa na wana sita, ambao majina yao ni haya; Azrikamu, na Bokeru, na Ishmaeli, na Shearia, na Obadia, na Hanani. Hao wote walikuwa wana wa Aseli

1 Mambo ya Nyakati 10

1 Basi Wafilisti wakapigana juu ya Israeli; nao watu wa Israeli wakakimbia mbele ya Wafilisti, wakaanguka wameuawa katika mlima Gilboa. 2 Nao Wafilisti wakamfuatia sana Sauli na wanawe; Wafilisti wakawaua Yonathani, na Abinadabu, na Malkishua, wana wa Sauli. 3 Tena vita vilikuwa vikali sana juu ya Sauli, na wapiga upinde wakampata; hata akafadhaika sana kwa sababu ya wapiga upinde. 4 Ndipo Sauli akamwambia yule mchukua silaha zake, Futa upanga wako, unichome nao, wasije watu hawa wasiotahiriwa wakanisimanga. Lakini huyo mchukua silaha zake akakataa; kwa sababu aliogopa sana. Basi Sauli akautwaa upanga wake, akauangukia. 5 Na mchukua silaha zake alipoona ya kuwa Sauli amekufa, yeye naye akauangukia upanga wake, akafa. 6 Hivyo Sauli akafa, na wanawe watatu; na nyumba yake yote wakafa pamoja. 7 Kisha watu wote wa Israeli, waliokuwa huko bondeni, walipoona ya kuwa wamekimbia, na ya kuwa Sauli na wanawe wamekufa, wakaiacha miji yao, wakakimbia; nao Wafilisti wakaenda wakakaa humo. 8 Hata ikawa siku ya pili yake Wafilisti walipokwenda kuwateka nyara hao waliouawa, walimwona Sauli na wanawe wameanguka juu ya mlima Gilboa. 9 Wakamvua mavazi, wakamtwalia kichwa, na silaha zake, kisha wakapeleka wajumbe kwenda nchi ya Wafilisti pande zote, ili kutangaza habari kwa sanamu zao, na kwa watu. 10 Wakaziweka silaha zake nyumbani mwa miungu yao, wakakikaza kichwa chake nyumbani mwa Dagoni. 11 Na watu wote wa Yabesh-gileadi waliposikia hayo yote Wafilisti waliyomtenda Sauli, 12 wakainuka mashujaa wote, wakautwaa mwili wake Sauli, na miili ya wanawe, wakaileta Yabeshi, wakaizika mifupa yao chini ya mwaloni huko Yabeshi, nao wakafunga muda wa siku saba. 13 Basi Sauli alikufa kwa sababu ya kosa lake alilomkosa Bwana, kwa sababu ya neno la Bwana, asilolishika; na tena kwa kutaka shauri kwa mwenye pepo wa utambuzi, aulize kwake, 14 asiulize kwa Bwana; kwa hiyo akamwua, na ufalme akamgeuzia Daudi, mwana wa Yese.

1 Mambo ya Nyakati 11

1 Ndipo Israeli wote wakamkusanyikia Daudi huko Hebroni, wakisema, Tazama, sisi tu mfupa wako na nyama yako. 2 Katika zamani za kale, hata hapo Sauli alipokuwa mfalme, wewe ndiwe uliyewatoa na kuwaingiza Israeli. Naye Bwana, Mungu wako, akakuambia, Ndiwe, utakayewalisha watu wangu Israeli, ndiwe utakayekuwa mkuu juu ya watu wangu Israeli. 3 Basi wazee wote wa Israeli wakamjia mfalme huko Hebroni; naye Daudi akafanya agano nao huko Hebroni mbele za Bwana; nao wakamtia Daudi mafuta, awe mfalme wa Israeli, sawasawa na neno la Bwana kwa mkono wa Samweli. 4 Kisha Daudi na Israeli wote wakaenda Yerusalemu, (ndio Yebusi;) nao Wayebusi, wenyeji wa nchi, walikuwamo. 5 Na hao wenyeji wa Yebusi wakamwambia Daudi, Hutaingia humu. Walakini Daudi akaitwaa ngome ya Sayuni; huu ndio mji wa Daudi. 6 Naye Daudi akasema, Mtu ye yote atakayekuwa wa kwanza wa kuwapiga Wayebusi, yeye atakuwa mkuu na jemadari. Naye wa kwanza aliyepanda ni Yoabu mwana wa Seruya, naye akawa mkuu. 7 Basi Daudi akakaa ngomeni; kwa hiyo huuita mji wa Daudi. 8 Akaujenga huo mji pande zote, toka Milo na kuuzunguka; naye Yoabu akautengeneza mji uliosalia. 9 Naye Daudi akaendelea, akazidi kuwa mkuu; kwa maana Bwana wa majeshi alikuwa pamoja naye. 10 Basi hawa ndio wakuu wa mashujaa aliokuwa nao Daudi, waliojitia nguvu pamoja naye katika ufalme wake, pamoja na Israeli wote, ili kumfanya awe mfalme, sawasawa na neno la Bwana alilonena juu ya Israeli. 11 Na hii ndiyo hesabu ya hao mashujaa aliokuwa nao Daudi; Yashobeamu, Mhakmoni, mkuu wa maakida; huyo aliuinua mkuki wake juu ya watu mia tatu, akawaua pamoja. 12 Na baada yake kulikuwa na Eleazari, mwana wa Dodai, Mwahohi, mmojawapo wa wale mashujaa watatu. 13 Huyo alikuwa pamoja na Daudi huko Pasdamimu; ndiko Wafilisti walikokusanyika vitani, palipokuwa na konde limejaa shayiri ;na hao watu wakakimbia mbele ya wafilisti. 14 Ndipo hao wakasimama katikati ya konde lile, wakalipigania, wakawaua Wafilisti; naye Bwana akafanya wokovu mkuu. 15 Tena, watatu miongoni mwa wale thelathini waliokuwa wakuu wakashuka mwambani, wakamwendea Daudi, hata pango la Adulamu; na jeshi la Wafilisti walikuwa wamefanya kambi bondeni mwa Warefai. 16 Na Daudi wakati ule alikuwako ngomeni, na walinzi wa Wafilisti wakati ule walikuwa huko Bethlehemu. 17 Naye Daudi akatamani, akasema, Laiti mtu angeninywesha maji ya kisima cha Bethlehemu, kilicho karibu na lango! 18 Basi hao watatu wakapenya jeshi la Wafilisti, wakateka maji kutoka kile kisima cha Bethlehemu, kilicho karibu na lango, wakayachukua, wakamletea Daudi; walakini Daudi hakukubali kuyanywa, akayamimina mbele za Bwana; 19 akasema, Mungu wangu apishe mbali, nisifanye hivi; je! Ninywe damu ya watu hao waliohatirisha nafsi zao? Maana kwa hatari ya nafsi zao wameyaleta. Kwa hiyo hakukubali kuyanywa. Hayo ndiyo waliyoyafanya wale mashujaa watatu. 20 Tena Abishai, nduguye Yoabu, alikuwa mkuu wa wale watatu; kwa kuwa aliuinua mkuki wake juu ya watu mia tatu, akawaua; akawa na jina kati ya wale watatu. 21 Katika wale watatu yeye alikuwa mwenye heshima kuliko hao wawili, akawa akida wao; ila hakudiriki kuwamo katika wale watatu. 22 Tena, Benaya, mwana wa Yehoyada, mtu hodari, wa Kabseeli, aliyekuwa amefanya mambo makuu, ndiye aliyewaua simba wakali wawili wa Moabu; pia akashuka ,akamwua simba katikati ya shimo wakati wa theruji. 23 Huyo akamwua Mmisri, mtu mrefu sana, aliyekuwa wa dhiraa tano urefu wake; na yule Mmisri alikuwa na mkuki kama mti wa mfumaji mkononi; lakini yeye akamshukia na gongo, akamnyakulia Mmisri mkuki mkononi, akamwua kwa mkuki wake mwenyewe. 24 Mambo hayo ndiyo aliyoyafanya Benaya, mwana wa Yehoyada, akawa na jina kati ya wale mashujaa watatu. 25 Tazama, alikuwa mwenye heshima kuliko wale thelathini, ila hakudiriki kuwamo katika wale watatu; naye Daudi akamweka juu ya walinzi wake. 26 Tena hawa ndio mashujaa wa majeshi ya askari; Asaheli nduguye Yoabu, Elhanani mwana wa Dodo wa Bethlehemu; 27 Shama Mharodi, Helesi Mpeloni; 28 Ira mwana wa Ikeshi Mtekoi, Abiezeri Mwanathothi; 29 Sibekai Mhushathi, Salmoni Mwahohi; 30 Maharai Mnetofathi, Heledi mwana wa Baana Mnetofathi; 31 Itai mwana wa Ribai wa Gibea wa wana wa Benyamini, Benaya Mpirathoni; 32 Hurai wa vijito vya Gaashi, Abieli Mwaibathi; 33 Azmawethi Mbaharumi, Eliaba Mshaalboni; 34 wana wa Yasheni Mgiloni, Yonathani mwana wa Shama Mharari; 35 Ahiamu mwana wa Sharari Mharari, Elifeleti mwana wa Ahasbai; Heferi 36 Mmaakathi, Ahia Mpeloni; 37 Hezro Mkarmeli, Paarai mwana wa Ezbai Mwarki; 38 Yoeli nduguye Nathani, Mibhari mwana wa Hagri; 39 Seleki Mwamoni, Naharai Mbeorothi, mchukua silaha wa Yoabu, mwana wa Seruya; 40 Ira Mwithri, Garebu Mwithri; 41 Uria Mhiti, Zabadi mwana wa Alai; 42 Adina mwana wa Shiza Mreubeni, mkuu wa Wareubeni, na thelathini pamoja naye; 43 Hanani mwana wa Maaka, na Yoshafati Mmithni; 44 Uzia Mwashterathi, Shama na Yeieli wana wa Hothamu Mwaroeri; 45 Yediaeli mwana wa Shimri, na Yoha nduguye, Muzi; 46 Elieli Mmahawi, na Yeribai, na Yoshavia, wana wa Elnaamu, na Ithma Mmoabi; 47 Elieli, na Obedi, na Yaasieli Mmesobai.

1 Mambo ya Nyakati 12

1 Basi hawa ndio wale waliomjia Daudi huko Siklagi, alipokuwa akijificha kwa ajili ya Sauli, mwana wa Kishi; nao walikuwamo miongoni mwa wale mashujaa, waliomsaidia vitani. 2 Walikuwa wenye kupinda upinde, nao walikuwa hodari wa kutumia mkono wa kuume na wa kushoto, kwa kutupa mawe ya teo, na kwa kupiga mishale ya upinde; walikuwa wa nduguze Sauli, wa Benyamini. 3 Mkubwa wao alikuwa Ahiezeri, kisha Yoashi, wana wa Shemaa Mgibeathi; na Yezieli, na Peleti, wana wa Azmawethi; na Beraka, na Yehu Mwanathothi; 4 na Ishmaya Mgibeoni, shujaa wa wale thelathini, naye alikuwa juu ya wale thelathini; na Yeremia, na Yahazieli, na Yohana, na Yozabadi Mgederathi; 5 Eluzai, na Yerimothi, na Bealia, na Shemaria, na Shefatia Mharufi; 6 Elkana, na Ishia, na Azaleli, na Yoezeri, na Yashobeamu, Wakora; 7 na Yoela, na Zebadia, wana wa Yerohamu, wa Gedori. 8 Na wa Wagadi wakajitenga kumfuata Daudi ngomeni huko nyikani, waume mashujaa, watu waliozoea vita, walioweza kutumia ngao na mkuki; ambao nyuso zao zilikuwa kama nyuso za simba, nao walikuwa wepesi kama kulungu juu ya milima; 9 Ezeri mkubwa wao, Obadia wa pili, Eliabu wa tatu; 10 Mishmana wa nne, Yeremia wa tano; 11 Atai wa sita, Elieli wa saba; 12 Yohana wa nane, Elzabadi wa kenda; 13 Yeremia wa kumi, Makbanai wa kumi na moja. 14 Hao wa wana wa Gadi walikuwa maakida wa jeshi, yeye aliyekuwa mdogo amelingana na mia, na yeye aliyekuwa mkuu, na elfu. 15 Hao ndio wale waliovuka Yordani katika mwezi wa kwanza, ulipofurika kingo zake zote; nao wakawakimbiza wote wa bondeni kuelekea mashariki na magharibi pia. 16 Tena wakafika ngomeni kwa Daudi baadhi ya wana wa Benyamini na Yuda. 17 Naye Daudi akatoka ili kuwalaki, akajibu, akawaambia, Kama mmenijia kwa amani ili kunisaidia, basi moyo wangu utaambatana nanyi; lakini kama mmekuja ili kunisaliti kwa adui zangu, kwa kuwa hamna udhalimu mikononi mwangu, Mungu wa baba zetu na alitazame neno hili, na kulikemea. 18 Ndipo roho ikamjilia Abishai, mkuu wa wale thelathini, naye akasema, Sisi tu watu wako, Ee Daudi; Na wa upande wako, Ee mwana wa Yese; Amani, naam, amani iwe kwako, Na amani iwe kwao wakusaidiao; Maana akusaidiye ndiye Mungu wako. Ndipo Daudi akawakaribisha, akawaweka wawe maakida wa kile kikosi. 19 Wa Manase pia wengine walimwangukia Daudi, alipokwenda pamoja na Wafilisti juu ya Sauli vitani, lakini hawakuwasaidia; kwani wale mabwana wa Wafilisti wakafanya shauri, wakamfukuza, wakisema, kwa hatari ya vichwa vyetu atamwangukia bwana wake Sauli. 20 Naye alipokuwa akienda Siklagi, wakamwangukia hawa wa Manase, Adna, na Yozabadi, na Yediaeli, na Mikaeli, na Yozabadi, na Elihu, na Silethai, maakida wa maelfu waliokuwa wa Manase. 21 Wakamsaidia Daudi juu ya kile kikosi kilichomshambulia; kwani walikuwa waume mashujaa wote, nao wakawa maakida jeshini. 22 Maana siku kwa siku humjia Daudi watu wa kumsaidia, hata wakapata kuwa jeshi kubwa, kama jeshi la Mungu. 23 Na hizi ni hesabu za vichwa vya watu wenye silaha za vita, waliokuja Hebroni kwa Daudi, ili kumgeuzia ufalme wa Sauli, sawasawa na neno la Bwana. 24 Wana wa Yuda, waliochukua ngao na mkuki, walikuwa elfu sita na mia nane, wenye silaha za vita. 25 Wa wana wa Simeoni, waume mashujaa wa vita, elfu saba na mia moja. 26 Wa wana wa Lawi, elfu nne na mia sita. 27 Na Yehoyada alikuwa kichwa cha mbari ya Haruni, na pamoja naye walikuwa elfu tatu na mia saba; 28 tena Sadoki, kijana shujaa, na wa nyumba ya babaye, maakida ishirini na wawili. 29 Na wa wana wa Benyamini nduguze Sauli, elfu tatu; kwani hata sasa walio wengi wao walikuwa wameuhifadhi uaminifu wao kwa nyumba ya Sauli. 30 Na wa wana wa Efraimu, ishirini elfu na mia nane, waume mashujaa, watu wenye sifa katika mbari za baba zao. 31 Na wa nusu kabila ya Manase, kumi na nane elfu, waliotajwa majina yao, ili waje kumtawaza Daudi awe mfalme. 32 Na wa wana wa Isakari, watu wenye akili za kujua nyakati, kuyajua yawapasayo Israeli wayatende; vichwa vyao walikuwa watu mia mbili na ndugu zao wote walikuwa chini ya amri yao. 33 Wa Zabuloni, watu wawezao kwenda pamoja na jeshi, hodari wa kupanga vita, wenye zana za vita za kila namna, hamsini elfu; askari wastadi wasiokuwa wenye moyo wa kusita-sita. 34 Na wa Naftali, maakida elfu, na pamoja nao watu wenye ngao na mkuki thelathini na saba elfu. 35 Na wa Wadani, watu hodari wa kupanga vita, ishirini na nane elfu na mia sita. 36 Na wa Asheri, watu wawezao kwenda pamoja na jeshi, hodari wa kupanga vita, arobaini elfu. 37 Tena, ng'ambo ya pili ya Yordani, wa Wareubeni, na wa Wagadi, na wa nusu kabila ya Manase, wenye zana za vita za kupigania za kila namna, mia na ishirini elfu. 38 Hao wote, watu wa vita, askari wastadi, wakaja Hebroni wenye moyo mkamilifu, ili kumtawaza Daudi awe mfalme juu ya Israeli wote; tena wote waliosalia wa Israeli nao walikuwa na moyo mmoja kwamba wamtawaze Daudi. 39 Nao walikuwako huko pamoja na Daudi siku tatu, wakila na kunywa; kwani ndugu zao walikuwa wamewaandalia tayari. 40 Zaidi ya hayo, wale waliokuwa karibu nao, hata mpaka kwa Isakari, na Zabuloni, na Naftali, wakaleta chakula juu ya punda, na ngamia, na nyumbu, na ng'ombe, vyakula vya unga, mikate ya tini, na vichala vya zabibu kavu, na divai, na mafuta, na ng'ombe, na kondoo tele; kwa kuwa kulikuwa na furaha katika Israeli.

1 Mambo ya Nyakati 13

1 Kisha Daudi akafanya shauri na maakida wa maelfu, na maakida wa mamia, naam, na kila kiongozi. 2 Daudi akawaambia jamii yote ya Israeli, Likiwa jema kwenu, tena likiwa limetoka kwa Bwana, Mungu wetu, na tutume watu huku na huku mahali pote kwa ndugu zetu waliosalia katika nchi yote ya Israeli, ambao pamoja nao makuhani na Walawi wamo ndani ya miji yao yenye viunga, ili wakusanyike kwetu; 3 nasi tujirudishie tena sanduku la Mungu wetu; maana hamkuuliza neno kwa hilo katika siku za Sauli. 4 Nao jamii nzima wakasema ya kwamba watafanya hivyo; kwa kuwa neno hilo lilikuwa jema machoni pa watu wote. 5 Basi Daudi akawakusanya Israeli wote, toka Shihori, kijito cha Misri, hata pa kuingilia Hamathi, ili kwamba walilete sanduku la Mungu kutoka Kiriath-yearimu. 6 Basi Daudi akapanda, yeye na Israeli wote, mpaka Baala, ndio Kiriath-yearimu, ulio wa Yuda, ili kulileta toka huko sanduku la Mungu, Bwana akaaye juu ya makerubi, lililoitwa kwa Jina lake. 7 Wakalipandisha sanduku la Mungu juu ya gari jipya kutoka nyumba ya Abinadabu; na Uza na Ahio wakaliendesha lile gari. 8 Wakacheza Daudi na Israeli wote, mbele za Mungu, kwa nguvu zao zote; na kwa nyimbo na kwa vinubi, na kwa vinanda, na kwa matari, na kwa matoazi, na kwa tarumbeta. 9 Hata walipofika penye uga wa Nakoni, Uza akaunyosha mkono wake alishike sanduku; kwa maana wale ng'ombe walikunguwaa. 10 Ndipo hasira ya Bwana ikawaka juu ya Uza, naye akampiga, kwa sababu alilinyoshea sanduku mkono wake, hata akafa pale pale mbele za Mungu. 11 Naye Daudi akaona uchungu, kwa kuwa Bwana amemfurikia Uza; akapaita mahali pale Peres-uza hata leo. 12 Naye Daudi akamwogopa Mungu siku ile, akasema, Nitajileteaje sanduku la Mungu kwangu? 13 Basi Daudi hakujichukulia sanduku mjini mwa Daudi, ila akalihamisha kando na kulitia nyumbani kwa Obed-edomu Mgiti. 14 Sanduku la Mungu likakaa na jamaa ya Obed-edomu, nyumbani mwake, muda wa miezi mitatu; naye Bwana akaibariki nyumba ya Obed-edomu, na yote aliyokuwa nayo.

1 Mambo ya Nyakati 14

1 Naye Hiramu, mfalme wa Tiro, akatuma wajumbe kwa Daudi, akampelekea na mierezi, na waashi, na maseremala, ili wamjengee nyumba. 2 Daudi akajua ya kwamba Bwana amemweka imara ili amiliki juu ya Israeli, kwa kuwa milki yake imeinuka kwa ajili ya watu wake Israeli. 3 Tena Daudi akazidi kuoa wake huko Yerusalemu; akazidi Daudi kuzaa wana na binti. 4 Na haya ndiyo majina ya watoto aliozaliwa huko Yerusalemu; Shamua, na Shobabu, na Nathani, na Sulemani; 5 na Ibhari, na Elishua, na Elpeleti; 6 na Noga, na Nefegi, na Yafia; 7 na Elishama, na Eliada, na Elifeleti. 8 Na waliposikia hao Wafilisti ya kwamba Daudi ametiwa mafuta ili awe mfalme juu ya Israeli wote, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akasikia, akatoka nje kupigana nao. 9 Basi hao Wafilisti walikuwa wamekuja na kuteka nyara katika bonde la Warefai. 10 Daudi akamwuliza Mungu, kusema, Je! Nipande juu ya Wafilisti! Utawatia mikononi mwangu? Naye Bwana akamwambia, Panda; kwa kuwa nitawatia mikononi mwako. 11 Basi wakapanda mpaka Baal-perasimu, Daudi naye akawapiga huko; Daudi akasema, Bwana amewafurikia adui zangu kwa mkono wangu, kama mafuriko ya maji. Basi wakapaita mahali pale jina lake Baal-perasimu. 12 Nao wakaiacha miungu yao huko; naye Daudi akaamuru, ikateketezwa kwa moto. 13 Lakini hao Wafilisti wakateka nyara tena mara ya pili bondeni. 14 Na Daudi akamwuliza Mungu tena; naye Mungu akamwambia, Hutapanda kuwafuata; uwageukie mbali, ukawajie huko kuielekea miforsadi. 15 Kisha itakuwa utakapoisikia sauti ya kwenda katika vilele vya miforsadi, ndipo utakapokwenda nje vitani; kwa maana ndipo Mungu ametoka mbele yako, awapige jeshi la Wafilisti. 16 Daudi akafanya kama vile Mungu alivyomwamuru; wakawapiga jeshi la Wafilisti toka Geba mpaka Gezeri. 17 Sifa za Daudi zikafika nchi zote; naye Bwana akawaletea mataifa yote hofu yake.

1 Mambo ya Nyakati 15

1 Basi Daudi akajifanyia nyumba katika mji wa Daudi; akapaweka tayari mahali kwa ajili ya sanduku la Mungu, akalipigia hema. 2 Ndipo Daudi akasema, Haimpasi mtu awaye yote kulichukua sanduku la Mungu, isipokuwa Walawi peke yao; kwa kuwa hao ndio aliowachagua Bwana, ili walichukue sanduku la Mungu, na kumtumikia daima. 3 Basi Daudi akawakusanya Israeli wote huko Yerusalemu, ili kulipandisha sanduku la Bwana, mpaka mahali pake alipoliwekea tayari. 4 Daudi akawakutanisha wana wa Haruni, na Walawi; 5 wa wana wa Kohathi; Urieli mkuu wao, na nduguze mia na ishirini; 6 wa wana wa Merari; Asaya mkuu wao, na nduguze mia mbili na ishirini; 7 wa wana wa Gershoni; Yoeli mkuu wao, na nduguze mia na thelathini; 8 wa wana wa Elsafani; Shemaya mkuu wao, na nduguze mia mbili; 9 wa wana wa Hebroni; Elieli mkuu wao, na nduguze themanini; 10 wa wana wa Uzieli; Aminadabu mkuu wao, na nduguze mia na kumi na wawili. 11 Tena, Daudi akawaita Sadoki na Abiathari makuhani, na hao Walawi, Urieli, Asaya, Yoeli, Shemaya, Elieli, na Aminadabu, 12 akawaambia, Ninyi ni vichwa vya mbari za baba za Walawi; jitakaseni, ninyi na ndugu zenu, ili mlipandishe sanduku la Bwana, Mungu wa Israeli, mpaka mahali pale nilipoliwekea tayari. 13 Kwani kwa sababu ninyi hamkulichukua safari ya kwanza, Bwana, Mungu wetu, alitufurikia, kwa maana hatukumtafuta sawasawa na sheria. 14 Basi makuhani na Walawi wakajitakasa, ili wapate kulipandisha sanduku la Bwana, Mungu wa Israeli. 15 Na wana wa Walawi wakalichukua sanduku la Mungu mabegani mwao kwa miti yake, kama vile Musa alivyoamuru, sawasawa na neno la Bwana. 16 Kisha Daudi akamwambia mkuu wa Walawi, kwamba awaagize ndugu zao waimbaji, pamoja na vyombo vyao vya kupigia ngoma, vinanda, na vinubi, na matoazi, wavipige na kupaza sauti kwa furaha. 17 Basi Walawi wakamwagiza Hemani mwana wa Yoeli; na wa nduguze, Asafu mwana wa Berekia; na wa wana wa Merari ndugu zao, Ethani mwana wa Kishi; 18 na pamoja nao ndugu zao kwa cheo cha pili, Zekaria, na Yaasieli, na Shemiramothi, na Yehieli, na Uni, na Eliabu; na Benaya, na Maaseya, na Matithia, na Elifelehu, na Mikneya, na Obed-edomu, na Yeieli, mabawabu. 19 Hivyo hao waimbaji, Hemani, Asafu, na Ethani, wakaagizwa kupiga matoazi yao ya shaba kwa sauti kuu; 20 na Zekaria, na Yaasieli na Shemiramothi, na Yehieli, na Uni, na Eliabu, na Maaseya, na Benaya, wenye vinanda vya sauti ya Alamothi; 21 na Matithiya, na Elifelehu, na Mikneya, na Obed-edomu, na Yeieli, na Azazia, wenye vinubi vya sauti ya Sheminithi, 22 waongoze. Na Kenania, mkuu wa Walawi, alikuwa juu ya uchukuzi; yeye aliusimamia uchukuzi, kwa sababu alikuwa mstadi. 23 Na Berekia na Elkana walikuwa mabawabu kwa ajili ya sanduku. 24 Na Shebania, na Yoshafati, na Nethaneli, na Amasai, na Zekaria, na Benaya, na Eliezeri, makuhani, wakapiga baragumu mbele ya sanduku la Mungu; na Obed-edomu na Yehia walikuwa mabawabu kwa ajili ya sanduku. 25 Basi Daudi, na wazee wa Israeli, na maakida wa maelfu, wakaenda, ili kulipandisha sanduku la agano la Bwana kutoka nyumbani mwa Obed-edomu kwa furaha kuu; 26 hata ikawa, Mungu alipowajalia Walawi waliolichukua sanduku la agano la Bwana, wakachinja ng'ombe saba, na kondoo waume saba. 27 Naye Daudi alikuwa amevaa joho ya kitani safi, na Walawi wote waliolichukua sanduku, na waimbaji, na Kenania msimamizi wa uchukuzi, na waimbaji; naye Daudi alikuwa amevaa naivera ya kitani. 28 Ndivyo Israeli wote walivyolipandisha sanduku la agano la Bwana kwa shangwe na kwa sauti ya tarumbeta, na kwa baragumu, na kwa matoazi, wakipiga sauti kuu kwa vinanda na vinubi. 29 Hata ikawa, sanduku la agano la Bwana lilipofika mjini kwa Daudi, Mikali binti Sauli akachungulia dirishani, akamwona mfalme Daudi, akicheza na kushangilia; akamdharau moyoni mwake.

1 Mambo ya Nyakati 16

1 Wakaliingiza sanduku la Mungu, na kuliweka katikati ya hema aliyoipiga Daudi kwa ajili yake; wakatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani mbele za Mungu. 2 Na Daudi alipokwisha kuitoa sadaka ya kuteketezwa na sadaka za amani, akawabariki watu kwa jina la Bwana. 3 Kisha akawagawia kila mtu wa Israeli, waume kwa wake, kila mtu mkate wa ngano, na kipande cha nyama, na mkate wa zabibu. 4 Akawaagiza baadhi ya Walawi kwamba watumike mbele ya sanduku la Bwana, wamfanyie ukumbusho, na shukrani, na sifa, Bwana, Mungu wa Israeli; 5 Asafu mkuu wao, na wa pili wake Zekaria, na Yeieli, na Shemiramothi, na Yehieli, na Matithiya, na Eliabu, na Benaya, na Obed-edomu, na Yeieli, wenye vinanda na vinubi; naye Asafu mwenye kupiga matoazi; 6 nao makuhani Benaya na Yahazieli wenye baragumu daima, mbele ya sanduku la agano la Mungu. 7 Ndipo siku hiyo Daudi alipoagiza kwanza kumshukuru Bwana, kwa mkono wa Asafu na nduguze. 8 Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake; Wajulisheni watu matendo yake. 9 Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi; Zitafakarini ajabu zake zote. 10 Jisifuni kwa jina lake takatifu; Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana. 11 Mtakeni Bwana na nguvu zake; Utafuteni uso wake siku zote. 12 Zikumbukeni ajabu zake alizozifanya; Miujiza yake na hukumu za kinywa chake; 13 Enyi wazao wa Israeli, mtumishi wake, Enyi wana wa Yakobo, wateule wake. 14 Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu; Duniani mwote mna hukumu zake. 15 Likumbukeni agano lake milele, Neno lile aliloviamuru vizazi elfu. 16 Agano alilofanya na Ibrahimu, Na uapo wake kwa Isaka; 17 Alilomthibitishia Yakobo kuwa amri, Na Israeli liwe agano la milele. 18 Akisema, Nitakupa wewe nchi ya Kanaani, Iwe urithi wenu mliopimiwa; 19 Mlipokuwa watu wawezao kuhesabiwa; Naam, watu wachache na wageni ndani yake. 20 Wakatanga-tanga toka taifa hata taifa, Toka ufalme mmoja hata kwa watu wengine. 21 Hakumwacha mtu awaonee; Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao; 22 Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu. 23 Mwimbieni Bwana, nchi yote; Tangazeni wokovu wake siku kwa siku. 24 Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, Na watu wote habari za maajabu yake. 25 Kwa kuwa Bwana ni mkuu mwenye kusifiwa sana; Na wa kuhofiwa kuliko miungu yote. 26 Maana miungu yote ya watu si kitu; Lakini Bwana ndiye aliyezifanya mbingu. 27 Heshima na adhama ziko mbele zake; Nguvu na furaha zipo mahali pake. 28 Mpeni Bwana, enyi jamaa za watu, Mpeni Bwana utukufu na nguvu. 29 Mpeni Bwana utukufu wa jina lake; Leteni sadaka, mje mbele zake; Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu; 30 Tetemekeni mbele zake, nchi yote. 31 Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie; Na waseme katika mataifa, Bwana ametamalaki; 32 Bahari na ivume na vyote viijazavyo; Mashamba na yashangilie na vyote vilivyomo; 33 Ndipo miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha, 34 Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 35 Nanyi mkaseme, Ee Mungu wa wokovu wetu, utuokoe, Utukusanye kwa kututoa katika mataifa, Tulishukuru jina lako takatifu, Tuzifanyie shangwe sifa zako. 36 Na ahimidiwe Bwana, Mungu wa Israeli, tangu milele hata milele. Na watu wote wakasema, Amina; wakamhimidi Bwana. 37 Basi akawaacha huko, mbele ya sanduku la agano la Bwana, Asafu na nduguze, ili watumike mbele ya sanduku daima, kila siku kama ilivyokuwa kazi yake. 38 Naye Obed-edomu, pamoja na ndugu zao, sitini na wanane; Obed-edomu na mwana wa Yeduthuni, na Hosa, wawe mabawabu; 39 na Sadoki kuhani, na nduguze makuhani, mbele ya maskani ya Bwana katika mahali pa juu palipokuwa huko Gibeoni, 40 ili kumtolea Bwana sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa daima asubuhi na jioni, naam, sawasawa na yote yaliyoandikwa katika torati ya Bwana, aliyowaamuru Israeli; 41 na pamoja nao Hemani na Yeduthuni, na wale wengine waliochaguliwa, waliotajwa majina yao, ili kumshukuru Bwana, kwa kuwa fadhili zake ni za milele; 42 na pamoja nao Hemani na Yeduthuni wenye baragumu na matoazi, kwa hao watakaovumisha sauti, na vinanda kwa ajili ya hizo nyimbo za Mungu; na hao wana wa Yeduthuni wawepo mlangoni. 43 Kisha watu wote wakaenda zao kila mtu nyumbani kwake; naye Daudi akarudi ili awabariki watu wa nyumbani mwake.

1 Mambo ya Nyakati 17

1 Ikawa, Daudi alipokuwa akikaa nyumbani mwake, Daudi akamwambia nabii Nathani, Angalia, mimi ninakaa katika nyumba ya mwerezi, bali sanduku la agano la Bwana linakaa chini ya mapazia. 2 Naye Nathani akamwambia Daudi, Haya, fanya yote yaliyomo moyoni mwako; kwa maana Mungu yu pamoja nawe. 3 Ikawa usiku uo huo, neno la Mungu likamjia Nathani, kusema, 4 Nenda, kamwambie mtumishi wangu, Daudi, Bwana asema hivi, Wewe hutanijengea nyumba ya kukaa; 5 kwa maana sikukaa ndani ya nyumba tangu siku ile nilipowaleta Israeli huku hata leo; lakini hema kwa hema nimehamia, na maskani kwa maskani. 6 Katika mahali mwote nilimokwenda na Israeli wote, je! Nimesema neno lo lote na mtu ye yote wa waamuzi wa Israeli, niliowaagiza kuwalisha watu wangu, nikisema, Mbona hamkunijengea nyumba ya mwerezi? 7 Basi sasa ndivyo utakavyomwambia mtumishi wangu Daudi, Bwana wa majeshi asema hivi, Nalikutwaa katika zizi la kondoo, katika kuwaandama kondoo ili uwe mkuu juu ya watu wangu Israeli; 8 nami nimekuwa pamoja nawe kila ulikokwenda, na kuwakatilia mbali adui zako wote mbele yako; nami nitakufanyia jina, kama jina la hao wakuu walioko duniani. 9 Tena nitawaagizia watu wangu Israeli mahali, nami nitawapanda, wapate kukaa mahali pao wenyewe, wasiondolewe tena; wala wana wa uovu hawatawatesa tena kama hapo kwanza, 10 na tangu siku ile nilipowaamuru waamuzi wawe juu ya watu wangu Israeli, nami nitawashinda adui zako wote. Pamoja na hayo nakuambia, ya kwamba Bwana atakujengea nyumba. 11 Hata itakuwa, siku zako zitakapotimia, uende na babazo, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayekuwa wa wana wako; nami nitaufanya imara ufalme wake. 12 Yeye ndiye atakayenijengea nyumba, nami nitakifanya imara kiti cha enzi cha ufalme wake milele. 13 Nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu; wala sitamwondolea fadhili zangu, kama nilivyomwondolea yeye aliyekuwa kabla yako; 14 ila nitamstarehesha katika nyumba yangu na katika ufalme wangu milele; na kiti chake cha enzi kitathibitishwa milele. 15 Kwa maneno hayo yote, na kwa maono hayo yote, ndivyo Nathani alivyonena na Daudi. 16 Ndipo akaingia Daudi mfalme, akaketi mbele za Bwana; akasema Mimi ni nani, Ee Bwana Mungu, na nyumba yangu ni nini, hata umenileta hata hapa? 17 Tena jambo hili lilikuwa dogo machoni pako, Ee Mungu; hata umeleta habari ya nyumba yangu mimi, mtumwa wako, kwa miaka mingi inayokuja, nawe umeniangalia sawasawa na hali ya mtu mwenye cheo, Ee Bwana Mungu. 18 Na Daudi akuambie nini tena zaidi kwa habari ya heshima aliyotendewa mtumwa wako? Kwa maana wewe umemjua mtumwa wako. 19 Ee Bwana, kwa ajili ya mtumwa wako, na kwa moyo wako mwenyewe, umeyatenda hayo makuu yote, ili yajulikane hayo matendo makuu yote. 20 Ee Bwana, hakuna mwingine kama wewe, wala hakuna Mungu mwingine ila wewe, kwa kadiri tulivyosikia kwa masikio yetu. 21 Tena ni taifa lipi duniani lililo kama watu wako Israeli, ambalo Mungu alikwenda kuwakomboa kwa ajili yake mwenyewe, ili wawe watu wake, na kujifanyia jina kwa njia ya mambo makuu, yenye kuogofya, kwa kufukuza mataifa mbele ya watu wako, uliowakomboa kutoka Misri? 22 Kwa maana watu wako Israeli ndio uliowafanya kuwa watu wako wa milele; nawe, Bwana, umekuwa Mungu wao. 23 Basi sasa, Ee Bwana, neno lile ulilolinena katika habari za mtumwa wako, na katika habari za nyumba yake, na lifanywe imara milele, ukafanye kama ulivyosema. 24 Jina lako na liwe imara, likatukuzwe milele, kusema, Bwana wa majeshi ndiye Mungu wa Israeli, naam, Mungu juu ya Israeli; na hiyo nyumba ya Daudi mtumwa wako imefanywa imara mbele zako. 25 Kwa kuwa wewe, Ee Mungu wangu, umenifunulia mimi mtumwa wako ya kuwa utanijengea nyumba; kwa hiyo mimi mtumwa wako nimeona vema moyoni mwangu kuomba mbele yako. 26 Na sasa, Ee Bwana, wewe ndiwe Mungu, nawe umemwahidia mtumwa wako jambo hili jema; 27 nawe sasa umekuwa radhi kuibarikia nyumba ya mtumwa wako, ipate kudumu milele mbele zako; kwa maana wewe, Bwana, umebarikia, nayo imebarikiwa milele.

1 Mambo ya Nyakati 18

1 Ikawa baadaye, Daudi akawapiga Wafilisti, akawashinda, akautwaa Gathi na vijiji vyake mikononi mwa Wafilisti. 2 Akapiga Moabu; na hao Wamoabi wakawa watumwa wa Daudi wakaleta zawadi. 3 Tena Daudi akampiga Hadadezeri, mfalme wa Soba, mpaka Hamathi, alipokwenda kujisimamishia mamlaka yake kwenye mto wa Frati. 4 Daudi akampokonya magari elfu, na wapanda farasi saba elfu, na askari waendao kwa miguu ishirini elfu; Daudi akawakata mshipa farasi wote wa magari, ila wa magari mia akawaweka. 5 Na Washami wa Dameski walipokuja wamsaidie Hadadezeri, mfalme wa Soba, Daudi akapiga katika hao Washami watu ishirini na mbili elfu. 6 Ndipo Daudi akaweka ngome katika Shamu ya Dameski; nao Washami wakawa watumwa wa Daudi, wakaleta zawadi. Naye Bwana akampa Daudi kushinda kila alikokwenda. 7 Tena Daudi akazitwaa ngao za dhahabu zilizovaliwa na watumishi wa Hadadezeri akazileta Yerusalemu. 8 Tena toka Tibhathi, na toka Berothai, miji ya Hadadezeri, Daudi akatwaa shaba nyingi mno, aliyofanyizia Sulemani ile bahari ya shaba, na zile nguzo, na vile vyombo vya shaba. 9 Hata aliposikia Tou, mfalme wa Hamathi, ya kuwa Daudi amewapiga jeshi lote la Hadadezeri, mfalme wa Soba, 10 akampeleka mwanawe Hadoramu kwa mfalme Daudi, ili kumsalimia, na kumbarikia, kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri, na kumpiga; kwa maana Hadadezeri alikuwa amepigana vita juu ya Tou; naye akaleta vyombo vya dhahabu, na fedha, na shaba, vya namna zote. 11 Hivi pia mfalme Daudi akavifanya wakfu kwa Bwana, pamoja na hiyo fedha na dhahabu, aliyoteka nyara kwa mataifa yote; kwa Edomu, na kwa Moabu, na kwa wana wa Amoni, na kwa Wafilisti, na kwa Amaleki. 12 Tena Abishai, mwana wa Seruya, akawapiga wa Waedomi katika Bonde la Chumvi watu kumi na nane elfu. 13 Akaweka ngome katika Edomu; na Waedomi wote wakawa watumwa wa Daudi. Naye Bwana akampa Daudi kushinda, kila alikokwenda. 14 Basi Daudi akatawala juu ya Israeli wote; akawafanyia hukumu na haki watu wake wote. 15 Na Yoabu mwana wa Seruya akawa juu ya jeshi; na Yehoshafati mwana wa Ahiludi mwenye kuandika tarehe. 16 Na Sadoki mwana wa Ahitubu, na Ahimeleki mwana wa Abiathari, walikuwa makuhani; na Shausha mwandishi; 17 na Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa juu ya Wakerethi na Wapelethi; na wana wa Daudi walikuwa wakuu kumzunguka mfalme.

1 Mambo ya Nyakati 19

1 Ikawa baada ya hayo, Nahashi, mfalme wa wana wa Amoni, akafa, akamiliki mwanawe mahali pake. 2 Naye Daudi akasema, Nitamtendea wema Hanuni, mwana wa Nahashi, kwa kuwa babaye alinitendea mimi wema. Basi Daudi akapeleka wajumbe ili kumtuliza kwa habari za babaye. Wakaja watumishi wa Daudi katika nchi ya wana wa Amoni kwa Hanuni, ili wamtulize. 3 Lakini wakuu wa wana wa Amoni wakamwambia Hanuni, Je! Waona Daudi amheshimu babayo kwa kukupelekea wafariji? Je! Hawakukujia watumishi wake ili kuiangalia nchi, na kuiangamiza, na kuipeleleza? 4 Basi Hanuni akawatwaa watumishi wa Daudi, akawanyoa, akawakatia nguo zao katikati, hata matakoni, akawatoa waende zao. 5 Wakaenda watu wakamwambia Daudi jinsi walivyotendewa wale watu. Naye akatuma watu kuwalaki; kwa sababu watu hao walikuwa wametahayarika sana. Mfalme akasema, Ngojeni Yeriko, hata mtakapoota ndevu zenu, ndipo mrudi. 6 Na wana wa Amoni walipoona ya kuwa wamekuwa machukizo kwa Daudi, Hanuni na wana wa Amoni wakapeleka talanta elfu za fedha ili kujiajiria magari na wapanda farasi kutoka Mesopotamia, na kutoka Atam-maaka, na kutoka Soba. 7 Basi wakajiajiria magari thelathini na mbili elfu, na mfalme wa Maaka na watu wake; nao walikuja wakatua mbele ya Medeba. Na wana wa Amoni wakakusanyika kutoka miji yao, wakaja vitani. 8 Basi Daudi aliposikia habari akamtuma Yoabu, na jeshi lote la mashujaa. 9 Wakatoka wana wa Amoni, wakapanga vita langoni pa mji; na hao wafalme waliokuja walikuwa peke yao uwandani. 10 Basi Yoabu alipoona ya kwamba uso wa vita umekuwa juu yake mbele na nyuma, akachagua baadhi ya wateule wote wa Israeli, akawapanga juu ya Washami. 11 Na hao watu waliosalia akawatia mikononi mwa Abishai, nduguye, nao wakajipanga juu ya wana wa Amoni. 12 Akasema, Wakiwa Washami ni hodari mno kwangu, ndipo wewe utanisaidia; lakini wana wa Amoni wakiwa ni hodari mno kwako, ndipo mimi nitakusaidia wewe. 13 Uwe hodari, tukajitie moyo mkuu kwa ajili ya watu wetu, na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; naye Bwana afanye yaliyo mema machoni pake. 14 Basi Yoabu, na watu waliokuwa pamoja naye, wakakaribia kupigana na Washami; nao wakakimbia mbele yake. 15 Na wana wa Amoni walipoona ya kwamba Washami wamekimbia, wakakimbia nao mbele ya Abishai, nduguye, wakaingia mjini. Ndipo Yoabu akaja Yerusalemu. 16 Na Washami walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, wakapeleka wajumbe, wakawavuta Washami walioko ng'ambo ya Mto, na Shobaki, jemadari wa jeshi la Hadadezeri, akawaongoza. 17 Alipoambiwa Daudi; akakusanya Israeli wote, akavuka Yordani, akawajia, akapanga vita juu yao. Basi Daudi alipopanga vita juu ya Washami, wakapigana naye. 18 Washami wakakimbia mbele ya Israeli; naye Daudi akawaua katika Washami watu wa magari saba elfu, na askari waendao kwa miguu arobaini elfu, akamwua na Shobaki, jemadari wa jeshi. 19 Na watumwa wa Hadadezeri walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, walifanya amani na Daudi, wakamtumikia; wala Washami hawakukubali kuwasaidia wana wa Amoni tena.

1 Mambo ya Nyakati 20

1 Hata ikawa, mwanzo wa mwaka mpya, wakati watokapo wafalme kwenda vitani, Yoabu akawaongoza mashujaa wa jeshi, akaiteka nyara nchi ya wana wa Amoni, akaja akauhusuru Raba. Lakini Daudi akakaa Yerusalemu. Naye Yoabu akaupiga Raba akauangamiza. 2 Kisha Daudi akamtwalia mfalme wao taji toka kichwani pake, akaona ya kwamba uzani wake ni talanta ya dhahabu, na kulikuwa na vito vya thamani ndani yake; akavikwa Daudi kichwani; akazitoa nyara za mji, nyingi sana. 3 Na hao watu waliokuwamo akawatoa, akawakata-kata kwa misumeno, na kwa sululu za chuma, na kwa mashoka. Ndivyo alivyofanya Daudi kwa miji yote ya wana wa Amoni. Nao wakarudi Yerusalemu Daudi na watu wote. 4 Ikawa baada ya hayo, kulitokea vita na Wafilisti huko Gobu; ndipo Sibekai, Mhushathi, alipomwua Safu, mmojawapo wa Warefai; nao wakashindwa. 5 Kulikuwa na vita tena na Wafilisti; na Elhanani, mwana wa Yairi akamwua Lahmi nduguye Goliathi, Mgiti ,ambaye mti wa mkuki wake ulikuwa kama mti wa mfumaji. 6 Kulikuwa na vita tena huko Gathi; ambapo palikuwa na mtu mrefu sana, mwenye vidole vya mikono na miguu ishirini na vinne, kila mguu sita, na kila mkono sita; naye alizaliwa na Mrefai. 7 Naye huyo alipowatukana Israeli, Yonathani, mwana wa Shama, nduguye Daudi, akamwua. 8 Hao walizaliwa kwake huyo Mrefai wa Gathi,nao wakaanguka kwa mkono wa Daudi , na kwa mkono wa watumishi wake.

1 Mambo ya Nyakati 21

1 Tena shetani akasimama juu ya Israeli, akamshawishi Daudi kuwahesabu Israeli. 2 Basi Daudi akamwambia Yoabu, na wakuu wa watu, Nendeni kawahesabu Israeli toka Beer-sheba mpaka Dani; mkanipashe habari, nipate kujua jumla yao. 3 Naye Yoabu akasema, Bwana na awaongeze watu wake mara mia hesabu yao ilivyo; lakini, bwana wangu mfalme, si wote watumishi wa bwana wangu? Mbona basi bwana wangu analitaka neno hili? Mbona awe sababu ya hatia kwa Israeli? 4 Lakini neno la mfalme likawa na nguvu juu ya Yoabu. Kwa hiyo Yoabu akaenda zake, akapita kati ya Israeli wote, akafika Yerusalemu. 5 Naye Yoabu akamtolea Daudi jumla ya hesabu ya watu. Na hao wote wa Israeli walikuwa watu elfu mara elfu, na mia elfu, wenye kufuta panga; na wa Yuda watu mia nne na sabini elfu, wenye kufuta panga. 6 Lakini Lawi na Benyamini hakuwahesabu miongoni mwao; kwa sababu neno la mfalme limemchukiza Yoabu. 7 Neno hilo likawa baya machoni pa Mungu; kwa hiyo akawapiga Israeli. 8 Naye Daudi akamwambia Mungu, Nimekosa sana, kwa kuwa nimelifanya jambo hili; lakini sasa uuondolee mbali, nakusihi, uovu wa mtumwa wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa. 9 Naye Bwana akanena na Gadi, mwonaji wake Daudi, akisema, 10 Nenda ukanene na Daudi, ukisema, Bwana asema hivi, Nakuwekea mambo matatu; katika haya ujichagulie moja, nikutendee hilo. 11 Basi Gadi akamwendea Daudi, akamwambia, Bwana asema hivi, Kubali upendavyo; 12 miaka mitatu ya njaa; au miezi mitatu kuangamia mbele ya adui zako, ukipatwa na upanga wa watesi wako; au siku tatu upanga wa Bwana, yaani tauni katika nchi, na malaika wa Bwana akiharibu kati ya mipaka yote ya Israeli. Haya basi ufikiri ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma. 13 Naye Daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na nianguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi sana; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu. 14 Basi Bwana akawaletea Israeli tauni; nao wakaanguka wa Israeli watu sabini elfu. 15 Naye Mungu akatuma malaika aende Yerusalemu ili auangamize; naye alipokuwa tayari kuangamiza, Bwana akatazama, akaghairi katika mabaya, akamwambia malaika aharibuye, Basi yatosha; sasa ulegeze mkono wako. Naye malaika wa Bwana akasimama karibu na kiwanja cha kupuria cha Arauna, Myebusi. 16 Daudi akainua macho yake, akamwona huyo malaika wa Bwana amesimama kati ya nchi na mbingu, naye alikuwa na upanga wazi mkononi, umenyoshwa juu ya Yerusakmu. Ndipo Daudi na wazee wakaanguka kifulifuli, nao wamevaa nguo za magunia. 17 Daudi akamwambia Mungu, Je! Si mimi niliyeamuru watu wahesabiwe? Naam, mimi ndimi niliyekosa, na kufanya yaliyo maovu sana; lakini kondoo hawa, wamefanya nini? Mkono wako, nakusihi, Ee Bwana, Mungu wangu, na uwe juu yangu, na juu ya nyumba ya babangu; wala si juu ya watu wako, hata wao wapigwe. 18 Ndipo huyo malaika wa Bwana akamwamuru Gadi kwamba amwambie Daudi, ya kuwa Daudi akwee, akamwinulie Bwana madhabahu katika kiwanja cha kupuria cha Arauna, Myebusi. 19 Basi Daudi akakwea sawasawa na neno la Gadi, alilolinena kwa jina la Bwana. 20 Arauna alipogeuka, na kumwona yule malaika, ndipo yeye na wanawe wanne waliokuwa pamoja naye wakajificha. Naye Arauna alikuwa akipura ngano. 21 Basi Daudi alipokuwa akimjia Arauna, Arauna akatazama, akamwona Daudi, akatoka katika kile kiwanja, akamsujudia Daudi kifulifuli hata nchi. 22 Ndipo Daudi akamwambia Arauna, Unipe mahali pa kiwanja hiki, ili kwamba nimjengee Bwana madhabahu hapa; kwa thamani yake kamili utanipa; ili kwamba tauni izuiliwe katika watu. 23 Arauna akamwambia Daudi, Ujitwalie, na bwana wangu mfalme na afanye yaliyo mema machoni pake; tazama, ng'ombe kwa sadaka za kuteketezwa, na vyombo vya kupuria kwa kuni, na ngano kwa sadaka ya unga, nazitoa; zote nazitoa. 24 Mfalme Daudi akamwambia Arauna, La, sivyo, lakini kweli nitazinunua kwa thamani yake kamili; kwani sitamtwalia Bwana kilicho chako, wala kutoa sadaka ya kuteketezwa isiyo na gharama. 25 Basi Daudi akampimia Arauna thamani ya mahali pale shekeli mia sita za dhahabu kwa uzani 26 Kisha Daudi akamjengea Bwana madhabahu huko, akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani, akamlingana Bwana; naye akamwitikia kutoka mbinguni kwa moto juu ya madhabahu hiyo ya sadaka ya kuteketezwa. 27 Bwana naye akamwamuru malaika; naye akaurudisha upanga wake alani mwake tena. 28 Wakati huo, Daudi alipoona ya kwamba Bwana amemwitikia katika kiwanja cha Arauna, Myebusi, ndipo hutoa dhabihu huko. 29 Kwa maana ile maskani ya Bwana, aliyoifanya Musa jangwani, na madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, vilikuwapo wakati huo mahali pa juu pa Gibeoni. 30 Wala Daudi hakuweza kwenda mbele yake ili kumwuliza Mungu; kwa sababu aliona hofu kwa ajili ya upanga wa yule malaika wa Bwana.

1 Mambo ya Nyakati 22

1 Ndipo Daudi akasema, Hii ndiyo nyumba ya Bwana Mungu, na hii ndiyo madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa kwa Israeli. 2 Basi Daudi akaamuru wakusanyike wageni waliokuwa katika nchi ya Israeli; akaweka waashi wachonge mawe ili kujenga nyumba ya Mungu. 3 Daudi akaweka akiba tele ya chuma kwa misumari ya tarabe za malango, na kwa mafungo; na ya shaba akiba tele isiyo na uzani; 4 na mierezi isiyo na idadi; kwa kuwa Wasidoni na watu wa Tiro wakamletea Daudi mierezi tele. 5 Daudi akasema, Sulemani mwanangu akali ni mchanga bado, na mwororo, nayo nyumba atakayojengewa Bwana haina budi kuwa nzuri mno, yenye sifa na yenye fahari katika nchi zote; kwa hiyo mimi nitaiwekea akiba. Basi Daudi akaweka akiba tele kabla hajafa. 6 Ndipo akamwita Sulemani mwanawe, akamwagiza amjengee Bwana, Mungu wa Israeli, nyumba. 7 Daudi akamwambia Sulemani mwanawe, Kwangu mimi nia yangu ilikuwa kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Bwana, Mungu wangu. 8 Lakini neno la Bwana likanijia, kusema, Wewe umemwaga damu nyingi, na vita vikubwa umevifanya; wewe hutajenga nyumba kwa ajili ya jina langu, kwa sababu umemwaga damu nyingi juu ya nchi machoni pangu; 9 tazama, utazaliwa mwana, atakayekuwa mtu wa kustarehe; nami nitamstarehesha mbele ya adui zake pande zote; kwani jina lake litakuwa Sulemani, nami nitawapa Israeli amani na utulivu siku zake ; 10 huyo ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu; naye atakuwa mwanangu, nami nitakuwa babaye; nami nitakifanya imara milele kiti cha ufalme wake juu ya Israeli. 11 Sasa mwanangu, Bwana na awe pamoja nawe; ukafanikiwe, na kuijenga nyumba ya Bwana, Mungu wako, kama alivyonena kwa habari zako. 12 Bwana na akupe busara na akili, akakuagizie juu ya Israeli; ili uishike torati ya Bwana, Mungu wako. 13 Ndipo utakapofanikiwa, ukiangalia kuzitenda amri, na hukumu, Bwana alizomwagizia Musa juu ya Israeli; uwe hodari, na wa moyo mkuu; usiogope wala usifadhaike. 14 Basi sasa, tazama, katika shida yangu, nimeiwekea akiba nyumba ya Bwana, talanta elfu mia za dhahabu, na talanta elfu elfu za fedha; na shaba na chuma isiyo na uzani; kwa vile zilivyo tele; miti tena na mawe nimeweka akiba, nawe utaweza kuongeza. 15 Tena kwako kuna mafundi wengi, wenye kuchonga na kufanyiza kazi ya mawe na miti, na kila aliye mstadi kwa kazi yo yote; 16 ya dhahabu, ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, hapana hesabu; basi inuka ushike kazi, naye Bwana na awe pamoja nawe. 17 Tena Daudi akawaamuru wakuu wote wa Israeli, kwamba wamsaidie Sulemani mwanawe, akisema, 18 Je! Si Bwana, Mungu wenu, aliye pamoja nanyi? Na kuwastarehesha pande zote? Kwa kuwa wenyeji wa nchi amewatia mkononi mwangu; nayo nchi imetiishwa mbele za Bwana, na mbele ya watu wake. 19 Basi sasa jitieni moyo na nia kumtafuta Bwana, Mungu wenu; inukeni basi, mkamjengee Bwana Mungu mahali patakatifu, ili kulileta sanduku la agano la Bwana, na vyombo vitakatifu vya Mungu, ndani ya nyumba itakayojengwa kwa ajili ya jina la Bwana.

1 Mambo ya Nyakati 23

1 Basi Daudi alikuwa mzee, ameshiba siku; akamtawaza mwanawe Sulemani awe mfalme juu ya Israeli. 2 Akawakusanya wakuu wote wa Israeli, pamoja na makuhani na Walawi. 3 Nao wakahesabiwa Walawi wenye miaka thelathini na zaidi; na jumla yao kwa vichwa, mtu kwa mtu, ikapata thelathini na nane elfu. 4 Katika hao ishirini na nne elfu walikuwa wa kusimamia kazi ya nyumba ya Bwana; na sita elfu walikuwa maakida na makadhi; 5 na elfu nne walikuwa mabawabu; na elfu nne walimsifu Bwana kwa vinanda, nilivyovifanya, alisema Daudi, vya kumsifia. 6 Basi Daudi akawagawanya kuwa zamu zao sawasawa na wana wa Lawi; Gershoni, Kohathi, na Merari. 7 Wa Wagershoni; Ladani, na Shimei. 8 Wana wa Ladani; Yehieli mkuu wao, na Zethamu, na Yoeli, watu watatu. 9 Wana wa Shimei; Shelomothi, na Hazieli, na Harani, watatu. Hao walikuwa vichwa vya mbari za baba za Ladani. 10 Na wana wa Shimei; Yahathi, na Zina, na Yeushi, na Beria. Hao wanne walikuwa wana wa Shimei. 11 Naye Yahathi alikuwa mkubwa wao, na Zina alikuwa wa pili; lakini Yeushi na Beria hawakuwa na wana wengi; basi wakawa mbari ya baba kwa kuhesabiwa pamoja. 12 Wana wa Kohathi; Amramu, Ishari, Hebroni, na Uzieli, watu wanne. 13 Wana wa Amramu; Haruni na Musa; naye Haruni akatengwa, ili ayatakase yaliyo matakatifu sana, yeye na wanawe milele, ili kufukiza uvumba mbele za Bwana, kumtumikia, na kubariki kwa jina lake, milele. 14 Lakini kwa habari za Musa, mtu wa Mungu, wanawe hutajwa miongoni mwa kabila ya Lawi. 15 Wana wa Musa; Gershomu na Eliezeri. 16 Wana wa Gershomu; Shebueli mkuu wao. 17 Na wana wa Eliezeri; Rehabia mkuu wao. Yeye Eliezeri hakuwa na wana wengine; lakini wana wa Rehabia walikuwa wengi sana. 18 Wana wa Ishari; Shelomithi mkuu wao. 19 Wana wa Hebroni; Yeria mkuu wao, Amaria wa pili, Yahazieli wa tatu, na Yekameamu wa nne. 20 Wana wa Uzieli; Mika mkuu wao, na Ishia wa pili. 21 Wana wa Merari; Mali na Mushi. Wana wa Mali; Eleazari, na Kishi. 22 Akafa Eleazari, wala hakuwa na wana, ila binti tu; na ndugu zao, wana wa Kishi, wakawaoa. 23 Wana wa Mushi; Mali, na Ederi, na Yeremothi, watu watatu. 24 Hao walikuwa wana wa Lawi, kwa kufuata mbari za baba zao, yaani, vichwa vya mbari za baba zao waliohesabiwa, kwa hiyo hesabu ya majina yao kwa vichwa, hao walioifanya kazi ya utumishi wa nyumba ya Bwana, wenye miaka ishirini na zaidi. 25 Kwa kuwa Daudi alisema, Bwana, Mungu wa Israeli, amewastarehesha watu wake; naye hukaa Yerusalemu milele; 26 wala Walawi hawahitaji tena kuichukua maskani, na vyombo vyake vyote kwa utumishi wake. 27 Maana kwa maneno ya mwisho ya Daudi, hao wana wa Lawi walihesabiwa, wenye miaka ishirini na zaidi. 28 Kwani kazi yao ilikuwa kuwangojea wana wa Haruni katika utumishi wa nyumba ya Bwana, nyuani, na vyumbani, na kwa kuvisafisha vitakatifu vyote, ndiyo kazi ya utumishi wa nyumba ya Mungu; 29 tena kazi ya mikate ya wonyesho, na ya unga mwembamba wa sadaka ya unga; ikiwa ni wa maandazi yasiyochachwa, au wa yale yaliyotokoswa, au wa yale yaliyookwa; na kazi ya kila namna ya kipimo na cheo; 30 nao wasimame kila asubuhi kumshukuru na kumsifu Bwana, na jioni vivyo hivyo; 31 na kumtolea Bwana sadaka zote za kuteketezwa, katika siku za sabato, za mwezi mpya, na za sikukuu zilizoagizwa, kwa hesabu kadiri ya agizo lake, daima mbele za Bwana; 32 tena walinde ulinzi wa hema ya kukutania, na ulinzi wa patakatifu, na ulinzi wa wana wa Haruni, ndugu zao, katika utumishi wa nyumba ya Bwana.

1 Mambo ya Nyakati 24

1 Na zamu za wana wa Haruni ni hizi. Wana wa Haruni; Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari. 2 Lakini hao Nadabu na Abihu walikufa kabla ya baba yao, wala hawakuwa na watoto; kwa hiyo Eleazari na Ithamari wakafanya ukuhani. 3 Akawagawanya Daudi, na Sadoki wa wana wa Eleazari, na Ahimeleki wa wana wa Ithamari, katika utumishi kwa kadiri ya usimamizi wao. 4 Wakaonekana wakuu wengi wa wana wa Eleazari kuliko wa wana wa Ithamari; wakagawanyika hivi; wa wana wa Eleazari kulikuwa na kumi na sita, waliokuwa wakuu wa mbari za baba zao; na wa wana wa Ithamari, sawasawa na mbari za baba zao, wanane. 5 Ndivyo walivyogawanyika kwa kura, wao kwa wao; kwani kulikuwa na wakuu wa patakatifu, na wakuu wa Mungu, wa wana wa Eleazari, na wa wana wa Ithamari pia. 6 Naye Shemaya, mwana wa Nethaneli, mwandishi, aliyekuwa wa Walawi, akawaandika mbele ya mfalme, na mbele ya wakuu, na Sadoki kuhani, na Ahimeleki, mwana wa Abiathari, na wakuu wa mbari za baba za makuhani, na za Walawi; ikatwaliwa ya Eleazari mbari moja ya baba, na moja ikatwaliwa ya Ithamari. 7 Kura ya kwanza ikamtokea Yehoiaribu, na ya pili Yedaya; 8 ya tatu Harimu, ya nne Seorimu; 9 ya tano Malkia, ya sita Miyamini; 10 ya saba Hakosi, ya nane Abia; 11 ya kenda Yeshua, ya kumi Shekania; 12 ya kumi na moja Eliashibu, ya kumi na mbili Yakimu; 13 ya kumi na tatu Hupa, ya kumi na nne Yeshebeabu; 14 ya kumi na tano Bilga, ya kumi na sita Imeri; 15 ya kumi na saba Heziri, ya kumi na nane Hapisesi; 16 ya kumi na kenda Pethahia, ya ishirini Ezekieli; 17 ya ishirini na moja Yakini, ya ishirini na mbili Gamuli; 18 ya ishirini na tatu Delaya, ya ishirini na nne Maazia. 19 Huu ndio usimamizi wao katika huduma yao, waingie nyumbani mwa Bwana kwa kadiri ya agizo lao, kwa mkono wa Haruni baba yao, kama Bwana, Mungu wa Israeli, alivyomwamuru. 20 Na wa wana wa Lawi, waliosalia; wa wana wa Amramu, Shebueli; wa wana wa Shebueli, Yedeya. 21 Wa Rehabia; wa wana wa Rehabia, Ishia mkuu wao. 22 Wa Waishari, Shelomothi; wa wana wa Shelomothi, Yahathi. 23 Na wana wa Hebroni; Yeria mkuu wao, Amaria wa pili, Yahazieli wa tatu, Yekameamu wa nne. 24 Wana wa Uzieli, Mika; wa wana wa Mika, Shamiri. 25 Nduguye Mika, Ishia; wa wana wa Ishia, Zekaria. 26 Wana wa Merari; Mali na Mushi; wana wa Yaazia; Beno. 27 Wana wa Merari; wa Yaazia; Beno, na Shohamu, na Zakuri, na Ibri. 28 Wa Mali; Eleazari, asiyekuwa na wana. 29 Wa Kishi; wana wa Kishi; Yerameeli. 30 Na wana wa Mushi; Mali, na Ederi, na Yeremothi. Hao ndio wana wa Walawi, kwa kufuata mbari za baba zao. 31 Hao nao wakatupiwa kura vile vile, kama ndugu zao wana wa Haruni, machoni pa Daudi mfalme, na Sadoki, na Ahimeleki, na wakuu wa mbari za baba za makuhani na za Walawi; mbari za baba za mkuu, vile vile kama za nduguye mdogo.

1 Mambo ya Nyakati 25

1 Tena Daudi na maakida wa jeshi wakatenga kwa utumishi baadhi ya wana wa Asafu, na wa Hemani, na wa Yeduthuni, watakaotabiri kwa vinubi na vinanda, na matoazi; hii ndiyo hesabu ya wafanya kazi sawasawa na utumishi wao; 2 wa wana wa Asafu; Zakuri, na Yusufu, na Nethania, na Asharela, wana wa Asafu; walioamriwa na Asafu, aliyetabiri kwa amri ya mfalme. 3 Wa Yeduthuni; wana wa Yeduthuni; Gedalia, na Seri, na Yeshaya, na Hashabia, na Matithia, [na Shimei], watu sita; walioamriwa na baba yao Yeduthuni mwenye kinubi, aliyetabiri katika kumshukuru na kumsifu Bwana. 4 Wa Hemani; wana wa Hemani; Bukia, Matania, Uzieli, Shebueli, na Yeremothi, Hanania, Hanani, Eliatha, Gidalti, na Romanti-ezeri, Yoshbekasha, Malothi, Hothiri, Mahaziothi; 5 hao wote ndio wana wa Hemani, mwonaji wa mfalme, kwa maneno ya Mungu, ili kuinua pembe. Naye Mungu akampa Hemani wana kumi na wanne na binti watatu. 6 Hao wote waliamriwa na baba yao, waimbe nyumbani mwa Bwana, wakiwa na matoazi, vinanda, na vinubi, kwa utumishi wa nyumba ya Mungu; Asafu, Yeduthuni, na Hemani wakiwa wanaamriwa na mfalme. 7 Na hesabu yao, pamoja na ndugu zao waliofundishwa kumwimbia Bwana, wote waliokuwa wastadi, walikuwa mia mbili na themanini na wanane. 8 Wakatupiwa kura ya ulinzi wao, sawasawa wote, mdogo kwa mkubwa, mwalimu kwa mwanafunzi. 9 Kura ya kwanza ikamtokea Yusufu, kwa Asafu; ya pili Gedalia; yeye na nduguze na wanawe, kumi na wawili; 10 ya tatu Zakuri, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 11 ya nne Seri, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 12 ya tano Nethania, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 13 ya sita Bukia, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 14 ya saba Asharela, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 15 ya nane Yeshaya, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 16 ya kenda Matania wanawe na nduguze, kumi na wawili; 17 ya kumi Shimei, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 18 ya kumi na moja Uzieli, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 19 ya kumi na mbili Hashabia, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 20 ya kumi na tatu Shebueli, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 21 ya kumi na nne Matithia, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 22 ya kumi na tano Yeremothi, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 23 ya kumi na sita Hanania, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 24 ya kumi na saba Yoshbekasha, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 25 ya kumi na nane Hanani, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 26 ya kumi na kenda Malothi, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 27 ya ishirini Eliatha, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 28 ya ishirini na moja Hothiri, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 29 ya ishirini na mbili Gidalti, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 30 ya ishirini na tatu Mahaziothi, wanawe na nduguze, kumi na wawili; 31 ya ishirini na nne Romanti-ezeri, wanawe na nduguze, kumi na wawili.

1 Mambo ya Nyakati 26

1 Kwa zamu zao mabawabu; wa Wakora; Meshelemia mwana wa Kore, wa wana wa Ebiasafu. 2 Naye Meshelemia alikuwa na wana; Zekaria mzaliwa wa kwanza, Yediaeli wa pili, Zebadia wa tatu, Yathnieli wa nne; 3 Elamu wa tano, Yohana wa sita, Elioenai wa saba. 4 Naye Obed-edomu alikuwa na wana; Shemaya mzaliwa wa kwanza, Yehozabadi wa pili, Yoa wa tatu, na Sakari wa nne, na Nethaneli wa tano; 5 Amieli wa sita, Isakari wa saba, Peulethai wa nane; kwa jinsi Mungu alivyombariki. 6 Naye mwanawe Shemaya akazaliwa wana, waliomiliki juu ya mbari ya baba yao; kwa kuwa walikuwa waume mashujaa. 7 Wana wa Shemaya; Othni, na Refaeli, na Obedi, na Elzabadi, nduguze walikuwa mashujaa, Elihu, na Semakia. 8 Hao wote walikuwa wana wa Obed-edomu; wao na wana wao na ndugu zao, watu hodari wawezao huo utumishi; watu wa Obed-edomu sitini na wawili. 9 Naye Meshelemia alikuwa na wana na nduguze, watu mashujaa, kumi na wanane. 10 Hosa naye, wa wana wa Merari, alikuwa na wana; Shimri mkuu wao; (kwani ajapokuwa yeye si mzaliwa wa kwanza, babaye alimweka mkuu); 11 Hilkia wa pili, Tebalia wa tatu, Zekaria wa nne; wana wote wa Hosa pamoja na nduguze walikuwa watu kumi na watatu. 12 Katika hao zilikuwa zamu za mabawabu, yaani, katika hao wakuu, wenye ulinzi sawasawa na ndugu zao, wa kutumika katika nyumba ya Bwana. 13 Nao wakatupiwa kura kwa ajili ya kila lango, wadogo sawasawa na wakubwa, kwa kadiri ya mbari za baba zao. 14 Kura ya mashariki ya lango ikamwangukia Meshelemia. Ndipo wakamtupia kura Zekaria mwanawe, mshauri mwenye busara; na kura yake ikamtokea ya kaskazini. 15 Ya Obed-edomu ya kusini; na ya wanawe nyumba ya akiba. 16 Ya Shupimu na Hosa upande wa magharibi, langoni pa Shalekethi, hapo penye daraja ya kupandia, ulinzi kwa ulinzi. 17 Upande wa mashariki walikuwapo Walawi sita, kaskazini wanne kila siku, kusini wanne kila siku, na wa nyumba ya akiba wawili wawili. 18 Penye Parbari upande wa magharibi, walikuwapo wanne darajani, na wawili huko Parbari. 19 Hizo ndizo zamu za mabawabu; wa wana wa Wakora, na wa wana wa Merari. 20 Na katika Walawi; Ahia alikuwa juu ya hazina za nyumba ya Mungu, na juu ya hazina za vitu vilivyowekwa wakfu. 21 Wana wa Ladani; wana wa Wagershoni waliokuwa wa Ladani; wakuu wa mbari za mababa waliokuwa wa Ladani, Mgershoni; Yehieli. 22 Wana wa Yehieli; Zethamu, na Yoeli nduguye, juu ya hazina za nyumba ya Bwana. 23 Wa Waamramu, wa Waishari, wa Wahebroni, wa Wauzieli; 24 na Shebueli, mwana wa Gershomu, mwana wa Musa, alikuwa mtawala hazina zote. 25 Na nduguze; wa Eliezeri, Rehabia mwanawe, na Ishia mwanawe, na Yoramu mwanawe, na Zikri mwanawe, na Shelomothi mwanawe. 26 Huyo Shelomothi na ndugu zake walikuwa juu ya hazina zote za vitu vilivyowekwa wakfu, alivyoviweka wakfu mfalme Daudi, na hao wakuu wa mbari za mababa, na maakida wa maelfu na wa mamia, na maakida wa jeshi. 27 Katika nyara zilizopatikana vitani, waliweka wakfu sehemu, ili kuitengeneza nyumba ya Bwana. 28 Na vyote alivyoviweka wakfu Samweli mwonaji, na Sauli mwana wa Kishi, na Abneri mwana wa Neri, na Yoabu mwana wa Seruya; na mtu ye yote aliyekiweka wakfu kitu cho chote, kilikuwa chini ya mkono wa Shelomothi na nduguze. 29 Katika Waishari, Kenania na wanawe walikuwa kwa ajili ya kazi ya nje juu ya Israeli, kuwa maakida na makadhi. 30 Katika Wahebroni, Hashabia na nduguze, mashujaa, elfu na mia saba, walikuwa na usimamizi juu ya Israeli ng'ambo ya Yordani upande wa magharibi; kwa ajili ya kazi zote za Bwana, na kwa utumishi wa mfalme. 31 Katika Wahebroni Yeria alikuwa mkuu, yaani, wa hao Wahebroni kwa kufuata vizazi vyao kwa mbari za mababa. Katika mwaka arobaini wa kutawala kwake Daudi wakatafutwa, wakaonekana huko Yazeri ya Gileadi miongoni mwao waume mashujaa. 32 Na nduguze, mashujaa, walikuwa elfu mbili na mia saba, wakuu wa mbari za mababa, ambao mfalme Daudi aliwaweka wawe wasimamizi juu ya Wareubeni, na Wagadi, na nusu kabila ya Wamanase, kwa ajili ya kila neno lililomhusu Mungu, na kwa mambo ya mfalme.

1 Mambo ya Nyakati 27

1 Basi wana wa Israeli kwa hesabu yao, wakuu wa mbari za mababa, na maakida wa maelfu na wa mamia, na wasimamizi wao waliomtumikia mfalme, kwa neno lo lote la zamu za kuingia na za kutoka mwezi kwa mwezi, miezi yote ya mwaka, wa kila zamu, walikuwa watu ishirini na nne elfu. 2 Juu ya zamu ya kwanza ya mwezi wa kwanza alikuwa Yashobeamu, mwana wa Zabdieli; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 3 Yeye alikuwa wa wana wa Peresi, mkuu wa maakida wote wa jeshi mwezi wa kwanza. 4 Na juu ya zamu ya mwezi wa pili alikuwa Dodai, Mwahohi, na zamu yake; na Miklothi alikuwa amiri; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 5 Akida wa tatu wa jeshi mwezi wa tatu alikuwa Benaya, mwana wa Yehoyada, kuhani; alikuwa mkuu, na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 6 Huyo Benaya ndiye yule aliyekuwa shujaa wa wale thelathini, na juu ya wale thelathini; na katika zamu yake alikuwa Amizabadi mwanawe. 7 Akida wa nne wa mwezi wa nne alikuwa Asaheli, nduguye Yoabu, na Zebadia mwanawe baada yake; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 8 Akida wa tano wa mwezi wa tano alikuwa Shamhuthi, Mwizrahi; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 9 Akida wa sita wa mwezi wa sita alikuwa Ira, mwana wa Ikeshi, Mtekoi; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 10 Akida wa saba wa mwezi wa saba alikuwa Heksi, Mpeloni, wa wana wa Efraimu; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 11 Akida wa nane wa mwezi wa nane alikuwa Sibekai, Mhushathi, wa Wazera; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 12 Akida wa kenda wa mwezi wa kenda alikuwa Abiezeri, Mwanathothi, wa Wabenyamini; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 13 Akida wa kumi wa mwezi wa kumi alikuwa Maharai, Mnetofathi, wa Wazera; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 14 Akida wa kumi na moja wa mwezi wa kumi na moja alikuwa Benaya, Mpirathoni, wa wana wa Efraimu; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 15 Akida wa kumi na mbili wa mwezi wa kumi na mbili alikuwa Heledi, Mnetofathi, wa Othnieli; na katika zamu yake walikuwa watu ishirini na nne elfu. 16 Tena wakuu wa kabila za Israeli walikuwa hawa; wa Wareubeni, Eliezeri mwana wa Zikri; wa Wasimeoni, Shefatia mwana wa Maaka; 17 wa Lawi, Hashabia mwana wa Kemueli; wa Haruni, Sadoki; 18 wa Yuda, Elihu, mmojawapo wa nduguze Daudi; wa Isakari, Omri mwana wa Mikaeli; 19 wa Zabuloni, Ishmaya mwana wa Obadia; wa Naftali, Yeromothi mwana wa Azrieli; 20 wa wana wa Efraimu, Hoshea mwana wa Azazia, wa nusu kabila ya Manase, Yoeli mwana wa Pedaya; 21 wa nusu kabila ya Manase katika Gileadi, Ido mwana wa Zekaria; wa Benyamini, Yaasieli mwana wa Abneri; 22 wa Dani, Azareli mwana wa Yerohamu. Hao walikuwa maakida wa kabila za Israeli. 23 Lakini Daudi hakufanya hesabu yao wenye miaka ishirini na waliopungua; kwa kuwa Bwana alikuwa amesema, ya kwamba atawaongeza Israeli mfano wa nyota za mbinguni. 24 Yoabu, mwana wa Seruya, akaanza kuhesabu, lakini hakumaliza; na ghadhabu ikawapata Israeli kwa hayo; wala haikuhesabiwa hesabu hiyo ndani ya taarifa za mfalme Daudi. 25 Na juu ya hazina za mfalme alikuwa Azmawethi mwana wa Adieli; na juu ya hazina za mashambani, za mijini, na vijijini, na ngomeni, alikuwa Yonathani mwana wa Uzia; 26 na juu ya hao wenye kazi ya shamba kuilima ardhi alikuwa Ezri mwana wa Kelubu; 27 na juu ya mashamba ya mizabibu alikuwa Shimei, Mramathi; na juu ya mazao ya mizabibu kwa ghala za mvinyo alikuwa Zabdi, Mshifmi; 28 na juu ya mizeituni na mikuyu iliyokuwamo katika Shefela alikuwa Baal-hanani, Mgederi; na juu ya ghala za mafuta alikuwa Yoashi; 29 na juu ya makundi ya ng'ombe waliolishwa katika Sharoni alikuwa Shitrai, Msharoni; na juu ya makundi waliokuwamo mabondeni alikuwa Shafati mwana wa Adlai; 30 na juu ya ngamia alikuwa Obili, Mwishmaeli; na juu ya punda alikuwa Yedeya, Mmeronothi; 31 na juu ya makundi ya kondoo alikuwa Yazizi, Mhagri. Hao wote walikuwa maakida wa akiba alizokuwa nazo mfalme Daudi. 32 Naye Yonathani, mjombawe Daudi, alikuwa mshauri, na mtu wa akili, na mwandishi; Yehieli mwana wa Hakmoni alikuwa pamoja na wana wa mfalme; 33 na Ahithofeli alikuwa mshauri wake mfalme; na Hushai, Mwarki, alikuwa rafiki yake mfalme; 34 na, baada ya Ahithofeli, walikuwa Yehoyada mwana wa Benaya, na Abiathari; na jemadari wa jeshi la mfalme alikuwa Yoabu.

1 Mambo ya Nyakati 28

1 Kisha Daudi akawakusanya huko Yerusalemu wakuu wote wa Israeli, wakuu wa kabila, na maakida wa vikosi wenye kumtumikia mfalme kwa zamu, na maakida wa maelfu, na maakida wa mamia, na wenye kutawala juu ya mali na milki za mfalme, na za wanawe, pamoja na matowashi, na mashujaa, naam, waume mashujaa wote. 2 Ndipo Daudi mfalme akasimama kwa miguu yake, akasema, Nisikilizeni, ndugu zangu, na watu wangu; Mimi nalikuwa na nia ya kuijenga nyumba ya kustarehe kwa ajili ya sanduku la agano la Bwana, na kiti cha kuwekea miguu yake cha Mungu wetu; hata nalikuwa nimeweka tayari kwa kujenga. 3 Lakini Mungu akaniambia, Wewe hutajenga nyumba kwa ajili ya jina langu, kwa sababu umekuwa mtu wa vita, nawe umemwaga damu. 4 Walakini Bwana, Mungu wa Israeli, alinichagua katika nyumba yote ya babangu kuwa mfalme juu ya Israeli milele, kwa kuwa amemchagua Yuda awe mkuu; na katika nyumba ya Yuda, alichagua nyumba ya babangu, na miongoni mwa wana wa babangu, aliniridhia mimi ili kunitawaza niwe mfalme juu ya Israeli wote; 5 tena katika wana wangu wote (kwani Bwana amenipa wana wengi), amemchagua Sulemani mwanangu ili aketi juu ya kiti cha enzi cha ufalme wa Bwana, juu ya Israeli. 6 Akaniambia, Sulemani, mwanao, ndiye atakayeijenga nyumba yangu na nyua zangu; kwa kuwa nimemchagua awe mwanangu, nami nitakuwa babaye. 7 Na ufalme wake nitauweka imara milele, akijitia kwa bidii kuzitenda amri zangu na hukumu zangu, kama hivi leo. 8 Basi sasa, machoni pa Israeli wote, hilo kusanyiko la Bwana, na masikioni pa Mungu wetu, angalieni na kuzitafuta amri zote za Bwana, Mungu wenu, ili mpate kuimiliki nchi hii njema, na kuwarithisha wana wenu baada yenu hata milele. 9 Nawe, Sulemani mwanangu, mjue Mungu wa baba yako, ukamtumikie kwa moyo mkamilifu, na kwa nia ya kumkubali; kwa kuwa Bwana hutafuta-tafuta mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira; ukimtafuta, ataonekana nawe; ukimwacha, atakutupa milele. 10 Jihadhari basi; kwani Bwana amekuchagua wewe ili ujenge nyumba itakayokuwa mahali patakatifu; uwe hodari ukatende hivyo. 11 Ndipo Daudi akampa Sulemani mwanawe mfano wa ukumbi wa hekalu, na nyumba zake, na hazina zake, na orofa zake, na vyumba vyake vya ndani, na mahali pa kiti cha rehema; 12 na mfano wa yote aliyokuwa nayo kwa roho, katika habari ya nyua za nyumba ya Bwana, na ya vyumba vyote vilivyoizunguka, ya hazina za nyumba ya Mungu, na ya hazina za vitu vilivyowekwa wakfu; 13 tena katika habari ya zamu za makuhani na Walawi, na ya kazi yote ya huo utumishi wa nyumba ya Bwana, na ya vyombo vyote vya utumishi nyumbani mwa Bwana; 14 ya dhahabu kwa uzani kwa vyombo vya dhahabu, kwa vyombo vyote vya utumishi wa kila namna; ya fedha kwa uzani kwa vyombo vyote vya fedha, kwa vyombo vyote vya utumishi wa kila namna; 15 kwa uzani tena kwa vinara vya dhahabu, na kwa taa zake za dhahabu, kwa uzani, kwa kila kinara, na kwa taa zake; na kwa vinara vya fedha, kwa uzani kwa kila kinara na kwa taa zake, kwa kadiri ya matumizi ya kila kinara; 16 na dhahabu kwa uzani kwa meza za mikate ya wonyesho, kwa kila meza; na fedha kwa meza za fedha; 17 na nyuma, na mabakuli, na vikombe vya dhahabu safi; na kwa matasa ya dhahabu, kwa uzani kwa kila tasa; na kwa matasa ya fedha, kwa uzani kwa kila tasa; 18 na kwa madhabahu ya kufukizia, dhahabu iliyosafika sana kwa uzani; na dhahabu kwa mfano wa gari, yaani, makerubi, yenye kutandaza mabawa, na kulifunika sanduku la agano la Bwana. 19 Hayo yote, akasema Daudi, yamenielea kwa maandiko kutoka kwa mkono wa Bwana, naam, kazi zote za mfano huu. 20 Kisha Daudi akamwambia Sulemani mwanawe, Uwe hodari, mwenye moyo mkuu, ukatende hivyo; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu, Mungu wangu, yu pamoja nawe; yeye hatakupungukia wala kukuacha, hata itakapomalizika kazi yote ya huo utumishi wa nyumba ya Bwana. 21 Na tazama, hizo zamu za makuhani na Walawi ziko, kwa utumishi wote wa nyumba ya Mungu; nao watakuwapo pamoja nawe kwa kazi ya kila namna, kila mtu mwenye hiari, aliye stadi kwa utumishi wo wote; tena maakida na watu wote watakuwa chini ya amri yako kabisa.

1 Mambo ya Nyakati 29

1 Kisha mfalme Daudi akawaambia kusanyiko lote, Sulemani mwanangu, ambaye Mungu amemchagua peke yake, akali ni mchanga bado na mwororo, nayo kazi hii ni kubwa; kwani nyumba hii ya enzi si kwa mwanadamu, ila kwa Bwana, Mungu. 2 Basi kwa uwezo wangu wote nimeiwekea akiba nyumba ya Mungu wangu, dhahabu kwa vitu vya dhahabu, na fedha kwa vitu vya fedha, na shaba kwa vitu vya shaba, na chuma kwa vitu vya chuma, na miti kwa vitu vya miti; vito vya shohamu, na vya kujazia, vito vya njumu, na vya rangi mbalimbali, na mawe ya thamani ya kila namna, na marimari tele. 3 Nami tena kwa kuwa nimeiwekea nyumba ya Mungu wangu shauku yangu, nami ninayo hazina yangu mwenyewe ya dhahabu na fedha, naitoa kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu, zaidi ya hiyo akiba niliyoiwekea tayari nyumba takatifu; 4 yaani, talanta elfu tatu za dhahabu, za dhahabu ya Ofiri, na talanta elfu saba za fedha iliyosafika, ya kuzifunikiza kuta za nyumba; 5 ya dhahabu, kwa vitu vya dhahabu, na ya fedha kwa vitu vya fedha, na kwa kazi za kila namna zitakazofanywa kwa mikono ya mafundi. Ni nani basi ajitoaye kwa moyo ili ajiweke wakfu leo kwa Bwana? 6 Ndipo wakuu wa mbari za mababa, na wakuu wa kabila za Israeli, na maakida wa maelfu na wa mamia, pamoja na wasimamizi wa kazi ya mfalme, wakajitoa kwa hiari yao; 7 nao wakatoa, kwa ajili ya utumishi wa nyumba ya Mungu, dhahabu talanta elfu tano, na darkoni elfu kumi,na fedha taranta elfu kumi, na shaba taranta elfu kumi na nane ,na chuma taranta elfu mia. 8 Na wale walioonekana kuwa na vito vya thamani wakavitoa vitiwe katika hazina ya nyumba ya Bwana, chini ya mkono wa Yehieli, Mgershoni. 9 Ndipo hao watu wakafurahi, kwa sababu wametoa kwa hiari yao wenyewe, kwa sababu kwa ukamilifu wa moyo, kwa hiari yao wenyewe, wamemtolea Bwana; mfalme Daudi naye akafurahi kwa furaha kuu. 10 Kwa hiyo Daudi akamhimidi Bwana, mbele ya mkutano wote; naye Daudi akasema, Uhimidiwe, Ee Bwana, Mungu wa Israeli baba yetu, milele na milele. 11 Ee Bwana, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu, na kushinda, na enzi; maana vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani ni vyako; ufalme ni wako, Ee Bwana, nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote. 12 Utajiri na heshima hutoka kwako wewe, nawe watawala juu ya vyote; na mkononi mwako mna uweza na nguvu; tena mkononi mwako mna kuwatukuza na kuwawezesha wote. 13 Basi sasa, Mungu wetu, twakushukuru na kulisifu jina lako tukufu. 14 Lakini mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kutoa kwa hiari hivi? Kwani vitu vyote vyatoka kwako na katika vitu vyako mwenyewe tumekutolea. 15 Kwani sisi tu wageni mbele zako, na wasafiri, kama walivyokuwa baba zetu wote; ni kama kivuli siku zetu duniani, wala taraji ya kukaa hapana. 16 Ee Bwana, Mungu wetu, akiba hii yote tuliyoiweka, ili tukujengee nyumba kwa ajili ya jina lako takatifu, yatoka yote mkononi mwako, na yote ni yako wewe. 17 Nami najua, Mungu wangu, ya kuwa wewe wajaribu moyo, nawe wapendezwa na unyofu. Nami katika unyofu wa moyo wangu nimeyatoa haya yote kwa hiari yangu mwenyewe; nami sasa nimeona kwa furaha watu wako, waliopo hapa, wakikutolea kwa hiari yao. 18 Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, baba zetu, ulilinde jambo hili milele katika fikira za mawazo ya mioyo ya watu wako, ukaiongoze mioyo yao kwako; 19 naye Sulemani mwanangu, umpe moyo mkamilifu, ili azishike amri zako, na shuhuda zako, na maagizo yako, akayatende hayo yote na kuijenga nyumba hii ya enzi, niliyoiwekea akiba. 20 Ndipo Daudi akawaambia kusanyiko lote, Haya, mhimidini Bwana, Mungu wenu. Basi kusanyiko lote wakamhimidi Bwana, Mungu wa baba zao, wakainama vichwa vyao, wakamsujudia Bwana, na mfalme naye. 21 Wakamtolea Bwana dhabihu, wakamchinjia Bwana sadaka za kuteketezwa, siku ya pili yake, yaani, ng'ombe elfu, na kondoo waume elfu, na wana-kondoo elfu, pamoja na sadaka zao za vinywaji, na dhabihu nyingi kwa ajili ya Israeli wote; 22 wakala na kunywa mbele za Bwana siku ile, kwa furaha kuu. Wakamtawaza Sulemani, mwana wa Daudi, mara ya pili, wakamtia mafuta mbele za Bwana, awe mkuu, na Sadoki awe kuhani. 23 Ndipo Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha Bwana, awe mfalme badala ya Daudi babaye, akafanikiwa; nao Israeli wote wakamtii. 24 Nao wakuu wote, na mashujaa, na wana wote wa mfalme Daudi nao, wakajitia chini ya mfalme Sulemani. 25 Naye Bwana akamtukuza Sulemani mno machoni pa Israeli wote, akampa fahari ya kifalme ya kumpita mfalme awaye yote aliyekuwa kabla yake katika Israeli. 26 Basi Daudi, mwana wa Yese, akawa mfalme juu ya Israeli wote. 27 Na wakati aliotawala juu ya Israeli, ulikuwa miaka arobaini; miaka saba alitawala Hebroni, na miaka thelathini na mitatu akatawala Yerusalemu. 28 Akafa mwenye umri mwema, ameshiba siku, na mali, na heshima; naye Sulemani mwanawe akamiliki badala yake. 29 Basi habari za mfalme Daudi, mwanzo na mwisho, angalia, zimeandikwa katika tarehe ya Samweli, mwonaji, na katika tarehe ya Nathani, nabii, na katika tarehe ya Gadi, mwonaji; 30 pamoja na kutawala kwake kote na nguvu zake, nazo zamani zilizompata yeye, na Israeli, na falme zote za nchi.

2 Mambo ya Nyakati 1

1 Basi Sulemani, mwana wa Daudi, alithibitishwa katika ufalme wake, naye Bwana, Mungu wake, alikuwa pamoja naye, akamtukuza mno. 2 Sulemani akasema na Israeli wote, na maakida wa maelfu, na wa mamia, na waamuzi, na kila shehe wa Israeli wote, wakuu wa nyumba za mababa. 3 Basi Sulemani akaenda mahali pa juu pa Gibeoni, na kusanyiko lote naye; kwani ndipo ilipokuwako hema ya kukutania ya Mungu, aliyoifanya Musa mtumishi wa Bwana jangwani. 4 Lakini sanduku la Mungu, Daudi alikuwa amelipandisha kutoka Kiriath-yearimu mpaka mahali Daudi alipolitengenezea; maana amelitandia hema katika Yerusalemu. 5 Tena madhabahu ya shaba, aliyoifanyiza Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, ilikuwako huko mbele ya maskani ya Bwana; Sulemani na kusanyiko wakaiendea. 6 Sulemani akaipandia huko madhabahu ya shaba mbele za Bwana, iliyokuwako hemani pa kukutania, akatoa sadaka elfu za kuteketezwa juu yake. 7 Usiku ule Mungu akamtokea Sulemani, akamwambia, Omba utakalo nikupe. 8 Sulemani akamwambia Mungu, Umemfanyia baba yangu Daudi fadhili kuu, nawe umenimilikisha mimi badala yake. 9 Basi sasa, Ee Bwana Mungu, na limyakinie baba yangu Daudi neno lako; maana umenitawaza niwe mfalme juu ya watu wengi kama mavumbi ya nchi. 10 Basi sasa nipe hekima na maarifa, nijue kutoka na kuingia mbele ya watu hawa; kwa kuwa ni nani awezaye kuwahukumu watu wako hawa walio wengi? 11 Naye Mungu akamwambia Sulemani, Kwa sababu neno hili lilikuwamo moyoni mwako, wala hukujitakia mali, wala utajiri, wala utukufu, wala maisha za wakuchukiao, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; bali umejitakia hekima na maarifa, upate kuwahukumu watu wangu, niliokutawaza juu yao; 12 basi hekima na maarifa umepewa; nami nitakupa mali, na utajiri, na utukufu, kupita walivyokuwa navyo wafalme wote waliokuwa kabla yako, wala baada yako hapatakuwa na mtu atakayekuwa navyo. 13 Akaja Sulemani kutoka mahali pa juu pa Gibeoni, toka mbele ya hema ya kukutania, mpaka Yerusalemu; akatawala juu ya Israeli. 14 Sulemani akakusanya magari na wapandao farasi; naye alikuwa na magari elfu na mia nne, na wapandao farasi kumi na mbili elfu, aliowaweka katika miji ya magari, na pamoja na mfalme huko Yerusalemu. 15 Mfalme akafanya fedha na dhahabu kuwa kama mawe humo Yerusalemu, na mierezi akaifanya kuwa kama mikuyu iliyomo Shefela, kwa kuwa mingi. 16 Nao farasi, aliokuwa nao Sulemani wakaletwa toka Misri; wakapewa wafanya biashara wake mfalme kwa makundi; kila kundi na thamani yake. 17 Nao hupandisha, na kuleta kutoka Misri gari kwa shekeli mia sita za fedha, na farasi kwa mia na hamsini, vivyo watu wakawaletea wafalme wote wa Wahiti, na wafalme wa Shamu, mikononi mwao.

2 Mambo ya Nyakati 2

1 Basi Sulemani alikusudia kujenga nyumba kwa jina la Bwana, na kuujengea ufalme wake nyumba. 2 Sulemani akahesabu watu sabini elfu wawe wachukuzi wa mizigo, na watu themanini elfu wawe wachongaji milimani, na elfu tatu na mia sita wawe wasimamizi wao. 3 Sulemani akatuma watu kwa Hiramu mfalme wa Tiro,akisema ,kama ulivyomtendea baba yangu Daudi, na kumletea mierezi , ajijengee nyumba ya kukaa ,unitendee na mimi. 4 Angalia, najenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wangu, ili kumfanyia wakfu, ya kufukizia mbele zake fukizo la manukato, na ya mkate wa wonyesho wa daima, na ya sadaka za kuteketezwa za asubuhi na jioni, na za siku za sabato, na za mwezi mpya, na za sikukuu zilizoagizwa za Bwana, Mungu wetu. Hili ni agizo la milele kwa Israeli. 5 Nayo nyumba nitakayoijenga ni kubwa; kwa sababu Mungu wetu ndiye mkuu juu ya miungu yote. 6 Lakini ni nani awezaye kumjengea nyumba, ikiwa mbingu hazimtoshi, wala mbingu za mbingu? Nami ni nani basi, hata nimjengee nyumba, isipokuwa kwa ajili ya kufukizia fukizo mbele zake? 7 Unipelekee basi mtu mstadi wa kazi ya dhahabu, na ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, na ya urujuani, na nyekundu, na samawi, mwenye kujua kuchora machoro, pamoja na wastadi walioko Yuda na Yerusalemu pamoja nami, aliowaweka baba yangu Daudi. 8 Niletee tena mierezi, na miberoshi, na miti ya msandali kutoka Lebanoni; maana najua ya kwamba watumishi wako hujua sana kuchonga miti Lebanoni; na tazama, watumishi wangu watakuwa pamoja na watumishi wako, 9 ili wanitengenezee miti kwa wingi; kwani nyumba nitakayoijenga itakuwa kubwa ajabu. 10 Na tazama, nitawapa watumishi wako, wachongaji wakatao miti, kori ishirini elfu za ngano iliyopondwa , na kori ishirini elfu za shayiri , na bathi ishirini elfu za mvinyo,na bathi ishirini elfu za mafuta. 11 Ndipo Hiramu mfalme wa Tiro akajibu kwa waraka, aliompelekea Sulemani, Ni kwa sababu Bwana awapenda watu wake, amekufanya uwe mfalme juu yao. 12 Hiramu akasema tena, Na ahimidiwe Bwana, Mungu wa Israeli, aliyezifanya mbingu na nchi, ambaye amempa mfalme Daudi mwana wa hekima, mwenye busara na akili, ili amjengee Bwana nyumba, na nyumba kwa ufalme wake. 13 Na sasa nimemtuma mtu mstadi, mwenye akili, yaani, Hiramu baba yangu. 14 mwana wa mwanamke wa binti za Dani, na babaye alikuwa mtu wa Tiro, ajuaye sana kazi ya dhahabu, na ya fedha, ya shaba, ya chuma, ya mawe, na ya mti, ya urujuani, ya samawi, na ya kitani safi, na ya nyekundu; tena mstadi wa kuchora machoro yo yote, na wa kufikiri fikira yo yote; apate kuagiziwa kazi pamoja na watu wako wastadi, tena na wastadi wa bwana wangu Daudi baba yako. 15 Basi sasa hiyo ngano na shayiri, mafuta na mvinyo, aliyonena bwana wangu, na wapelekewe watumishi wake; 16 nasi tutakata miti katika Lebanoni, kadiri utakavyohitaji; na kukuletea tukiieleza baharini mpaka Yafa; nawe utaichukua Yerusalemu. 17 Ndipo Sulemani akawahesabu wageni wote waliokuwamo katika nchi ya Israeli, sawasawa na hesabu aliyowahesabu Daudi baba yake; wakatokea mia hamsini na tatu elfu, na mia sita. 18 Akaweka katika hao sabini elfu wawe wachukuzi wa mizigo, na themanini elfu wawe wachongaji milimani, na wasimamizi elfu tatu na mia sita, ili wawatie watu kazini.

2 Mambo ya Nyakati 3

1 Ndipo Sulemani akaanza kuijenga nyumba ya Bwana huko Yerusalemu, juu ya mlima Moria, pale Bwana alipomtokea Daudi babaye alipotengeza mahali pale alipoagiza Daudi, katika kiwanja cha kupuria cha Arauna Myebusi. 2 Akaanza kujenga siku ya pili ya mwezi wa pili katika mwaka wa nne wa kutawala kwake. 3 Basi hii ndiyo misingi ya majengo ya nyumba ya Mungu aliyoiweka Sulemani. Urefu wake kwa mikono ya cheo cha kwanza ulikuwa mikono sitini, na upana wake mikono ishirini. 4 Na ukumbi uliokuwa mbele yake, urefu wake kadiri ya upana wa nyumba ulikuwa mikono ishirini, na kwenda juu kwake mia na ishirini; akaufunikiza ndani kwa dhahabu safi. 5 Nayo nyumba kubwa akaifunika miti ya miberoshi, aliyoifunikiza kwa dhahabu safi, akaifanyizia mitende na minyororo. 6 Akaipamba nyumba kwa vito iwe na uzuri; nayo dhahabu ilikuwa dhahabu ya Parvaimu. 7 Tena, akaifunikiza kwa dhahabu nyumba, na boriti, na vizingiti, na kuta zake, na milango yake; akachora makerubi kutani. 8 Akaifanya nyumba ya patakatifu pa patakatifu; urefu wake kadiri ya upana wa nyumba, ulikuwa mikono ishirini, na upana wake mikono ishirini; akaifunikiza kwa dhahabu safi, ya talanta mia sita. 9 Na uzani wa misumari ulikuwa shekeli hamsini za dhahabu. Akazifunikiza orofa zake za juu kwa dhahabu. 10 Na ndani ya nyumba ya patakatifu pa patakatifu akafanyiza makerubi mawili ya kuchonga; wakayafunikiza kwa dhahabu. 11 Na mabawa ya makerubi hayo urefu wake ulikuwa mikono ishirini; bawa moja mikono mitano, likiufikilia ukuta wa nyumba; na bawa la pili mikono mitano, likishikana na bawa la kerubi la pili. 12 Na bawa la kerubi la pili lilikuwa mikono mitano, likiufikilia ukuta wa nyumba; na bawa la pili mikono mitano, likishikana na bawa la kerubi la kwanza. 13 Yakaenea mabawa ya makerubi hayo mikono ishirini; yakasimama juu ya miguu yao, na nyuso zao ziliielekea nyumba. 14 Akalifanya pazia la samawi na urujuani na nyekundu, na kitani safi, akaifanyizia makerubi. 15 Tena akafanya mbele ya nyumba nguzo mbili za mikono thelathini na tano kwenda juu kwake, na taji iliyokuwa juu yake moja moja ilikuwa mikono mitano. 16 Akafanya minyororo ndani ya chumba cha ndani, akaiweka juu ya vichwa vya nguzo; akafanya makomamanga mia, akayaweka juu ya hiyo minyororo. 17 Akazisimamisha nguzo hizo mbele ya hekalu, moja upande wa kuume, na ya pili upande wa kushoto; akaliita jina la ile ya kuume Yakini, na jina la ile ya kushoto Boazi.

2 Mambo ya Nyakati 4

1 Tena akafanya madhabahu ya shaba, mikono ishirini urefu wake, na mikono ishirini upana wake, na mikono kumi kwenda juu kwake. 2 Tena akaifanya bahari ya kusubu, mikono kumi toka ukingo hata ukingo, ya mviringo, na kwenda juu kwake ilikuwa mikono mitano; na uzi wa mikono thelathini kuizunguka kabisa. 3 Na chini yake palikuwa na mifano ya ng'ombe, walioizunguka pande zote ,kwa mikono kumi,wakiizunguka pande zote ile bahari. Ng`ombe walikuwa safu mbili ,wakayeyushwa hapo ilipoyeyushwa hiyo bahari. 4 Ikakaa juu ya ng'ombe kumi na wawili, watatu wakitazama kaskazini, na watatu wakitazama magharibi, na watatu wakitazama kusini, na watatu wakitazama mashariki; na bahari iliwekwa juu yao, na pande zao za nyuma zote zilikuwa ndani. 5 Na unene wake ulikuwa nyanda nne, na ukingo wake ukafanywa kama ukingo wa kikombe, kama ua la yungi; huingia bathi elfu tatu, kukaa ndani yake. 6 Akafanya na birika kumi, akaziweka tano upande wa kuume, na tano upande wa kushoto, za kuoshea; ndizo walizooshea mambo ya kafara; lakini hiyo bahari ilikuwa ya makuhani ya kuogea. 7 Akavifanya vinara vya taa kumi vya dhahabu, kadiri ya vilivyoagiziwa; akavitia hekaluni, vitano upande wa kuume, na vitano upande wa kushoto. 8 Akafanya na meza kumi, akazitia hekaluni, tano upande wa kuume, na tano upande wa kushoto. Kisha akafanya mabakuli mia ya dhahabu. 9 Tena akaufanya ua wa makuhani, na ua mkubwa, nayo milango yake, akaifunikiza kwa shaba milango yake. 10 Nayo bahari akaiweka upande wa kuume kwa mashariki, kuelekea kusini. 11 Na Huramu akayafanya masufuria, na majembe, na mabakuli. Basi Huramu akamaliza kufanya hiyo kazi, aliyomfanyia mfalme Sulemani ya nyumba ya Mungu; 12 zile nguzo mbili, na vimbe, na taji mbili zilizokuwa juu ya nguzo; nazo nyavu mbili za kuzifunika vimbe mbili za taji zilizokuwa juu ya nguzo; 13 na makomamanga mia nne ya nyavu mbili; safu mbili za makomamanga kwa kila wavu, kuzifunika vimbe mbili za taji zilizokuwa juu ya nguzo. 14 Akayafanya na matako, na mabirika akafanya juu ya matako; 15 bahari moja, na ng'ombe kumi na wawili chini yake. 16 Masufuria pia, na majembe, na nyuma, na vyombo vyake vyote, Huramu akamfanyia mfalme Sulemani kwa nyumba ya BWANA ,vya shaba iliyokatuka. 17 Katika uwanda wa Yordani ndipo mfalme alipovisubu, katika udongo mzito kati ya Sukothi na Sereda. 18 Ndivyo alivyovifanya Sulemani vyombo hivyo vyote, vingi sana; kwa kuwa uzani wa shaba ulikuwa hautafutikani. 19 Basi Sulemani akavifanya vyombo vyote vilivyokuwamo nyumbani mwa Mungu, madhabahu ya dhahabu pia, nazo meza, ambazo juu yake iliwekwa mikate ya wonyesho; 20 na vinara na taa zake, ziwake kama ilivyoagizwa mbele ya chumba cha ndani, vya dhahabu iliyosafika; 21 na maua, na taa, na makoleo, ya dhahabu, ndiyo dhahabu bora; 22 na mikasi, na mabakuli, na miiko, na vyetezo, vya dhahabu iliyosafika; na kwa habari za mahali pa kuingia nyumbani, milango yake ya ndani ya patakatifu pa patakatifu, na milango ya nyumba, yaani ya hekalu, ilikuwa ya dhahabu.

2 Mambo ya Nyakati 5

1 Hivyo ikaisha kazi yote Sulemani aliyoifanyia nyumba ya Bwana. Sulemani akaviingiza vitu alivyovitakasa baba yake Daudi; fedha, na dhahabu, na vyombo vyote, akavitia ndani ya hazina za nyumba ya Mungu. 2 Ndipo Sulemani alipowakusanya wazee wa Israeli, na wakuu wote wa kabila, wakuu wa mbari za mababa wa wana wa Israeli, huko Yerusalemu, ili walipandishe sanduku la agano la Bwana kutoka mji wa Daudi, yaani, Sayuni. 3 Wakakutana watu wote wa Israeli mbele ya mfalme wakati wa sikukuu, katika mwezi wa saba. 4 Wakaja wazee wote wa Israeli, nao Walawi wakajitwika sanduku. 5 Wakalipandisha sanduku, na ile hema ya kukutania, na vyombo vitakatifu vyote vilivyokuwamo Hemani, vitu hivyo makuhani Walawi wakavipandisha. 6 Mfalme Sulemani, na mkutano wote wa Israeli, waliokutanika kwake, walikuwako mbele ya sanduku, wakichinja dhabihu za kondoo na ng'ombe, wasiohesabika wala kujumlishwa kwa kuwa wengi. 7 Makuhani wakaliingiza sanduku la agano la Bwana mahali pake katika chumba cha ndani cha nyumba, patakatifu pa patakatifu, yaani, chini ya mabawa ya makerubi. 8 Kwa maana makerubi yalinyosha mabawa yao juu ya mahali pa sanduku, makerubi yakalifunika lile sanduku na miti yake kwa juu. 9 Na ile miti ilikuwa mirefu, hata ncha za miti zilionekana sandukuni mbele ya chumba cha ndani, lakini hazikuonekana nje; nayo iko kuko huko hata leo. 10 Hamkuwa na kitu ndani ya sanduku, ila zile mbao mbili alizozitia Musa huko Horebu, Bwana alipofanya agano na wana wa Israeli, hapo walipotoka Misri. 11 Ikawa makuhani walipokwisha kutoka katika patakatifu; (kwani makuhani wote waliokuwapo, walikuwa wamejitakasa, wala hawakuzishika zamu zao; 12 tena Walawi waimbaji, wote pia, yaani Asafu, na Hemani, na Yeduthuni, na wana wao, na ndugu zao, hali wamevaa kitani safi, wenye matoazi na vinanda na vinubi, wamesimama upande wa mashariki wa madhabahu, na pamoja nao makuhani mia na ishirini wakipiga panda;) 13 hata ikawa, wenye panda na waimbaji walipokuwa kama mmoja, wakisikizisha sauti moja ya kumsifu na kumshukuru Bwana nao wakipaza sauti pamoja na panda na matoazi na vinanda, wakimsifu Bwana, wakisema, Kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele; ndipo nyumba ikajawa na wingu, naam, nyumba ya Bwana, 14 hata makuhani hawakuweza kusimama ili kufanya huduma yao, kwa sababu ya lile wingu; kwa kuwa nyumba ya Mungu imejaa utukufu wa Bwana.

2 Mambo ya Nyakati 6

1 Ndipo Sulemani akanena, Bwana alisema ya kwamba atakaa katika giza nene. 2 Lakini nimekujengea nyumba ya kukaa, iwe mahali pa makao yako milele. 3 Mfalme akageuza uso wake, akawabarikia mkutano wote wa Israeli; na mkutano wote wa Israeli wakasimama. 4 Akasema, Bwana, Mungu wa Israeli, ahimidiwe, aliyenena kwa kinywa chake na baba yangu Daudi, akalitimiza kwa mikono yake, akasema, 5 Tangu siku ile nilipowatoa watu wangu katika nchi ya Misri, sikuchagua mji wo wote wa kabila zote za Israeli ili kujenga nyumba, jina langu liwe humo; wala sikumchagua mtu ye yote awe mkuu juu ya watu wangu Israeli; 6 lakini nimeuchagua Yerusalemu, jina langu liwe humo; na Daudi nimemchagua awe juu ya watu wangu Israeli. 7 Basi ilikuwa moyoni mwake Daudi, baba yangu, kujenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wa Israeli. 8 Lakini Bwana akamwambia Daudi baba yangu, Kwa kuwa ilikuwa moyoni mwako kujenga nyumba kwa jina langu, ulifanya vema kuwaza hivi moyoni mwako; 9 lakini si wewe utakayeijenga nyumba hiyo; ila mwanao atakayetoka katika viuno vyako, yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu. 10 Basi Bwana amelitimiza neno lile alilolinena; nami nimesimama mahali pa Daudi baba yangu, na kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli, kama Bwana alivyoahidi, nami nimeijenga nyumba kwa jina la Bwana, Mungu wa Israeli. 11 Ndimo nilimoliweka hilo sanduku, ambalo ndani yake mna agano la Bwana, alilolifanya na wana wa Israeli. 12 Akasimama mbele ya madhabahu ya Bwana, machoni pa mkutano wote wa Israeli, akainyosha mikono; 13 (maana Sulemani alikuwa amefanya mimbari ya shaba, urefu wake mikono mitano, na upana wake mikono mitano, na kwenda juu kwake mikono mitatu, na kuisimamisha katikati ya ua; akasimama juu yake, akapiga magoti mbele ya mkutano wote wa Israeli, akaikunjua mikono yake kuelekea mbinguni); 14 akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe, mbinguni, wala duniani; ushikaye maagano na rehema kwa watumishi wako, waendao mbele zako kwa moyo wao wote; 15 uliyemtimizia mtumishi wako Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidi; naam, ulinena kwa kinywa chako, ukayatimiza kwa mkono wako, kama ilivyo leo. 16 Sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, umfikilizie mtumishi wako Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidia, ukisema, Hutakosa kuwa na mtu machoni pangu, wa kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli; wakiwa tu watoto wako wataiangalia njia yao, ili kuiendea torati yangu, kama wewe ulivyokwenda mbele zangu. 17 Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ulithibitishe neno lako, ulilomwambia mtumishi wako Daudi. 18 Lakini Mungu je! Yamkini atakaa na watu duniani? Tazama, mbingu na mbingu za mbingu za mbingu hazikutoshi; siuze nyumba hii niliyoijenga! 19 Walakini umwangalie mtumwa wako anayoyaomba, na kusihi, Ee Bwana, Mungu wangu, usikie kilio na maombi anayoyaomba mtumwa wako mbele zako; 20 ili macho yako yafumbuke kwa nyumba hii mchana na usiku, mahali uliponena, ndipo utakapoliweka jina lako; usikie maombi atakayoomba mtumwa wako, akikabili mahali hapa. 21 Uyasikie atakayosihi mtumwa wako, na watu wako Israeli, watakapoomba wakikabili mahali hapa; naam, usikie toka makaoni mwako, toka mbinguni, nawe usikiapo, samehe. 22 Ikiwa mtu amemkosea mwenzake, akitiwa kiapo, aapishwe, naye akija na kuapa hapa mbele ya madhabahu yako nyumbani humu; 23 basi, usikie mbinguni, ukatende, ukawahukumu watumwa wako; ukimlipiza mwovu, kumpatilizia njia yake kichwani; ukamfanyie haki mwenye haki, ukimjalia kwa kadiri ya haki yake. 24 Ikiwa watu wako Israeli wamepigwa mbele ya adui zao, kwa sababu wamekukosa wewe; kama wakirejea kwako, na kulikiri jina lako, wakikuomba na kukusihi nyumbani humu; 25 basi usikie huko mbinguni, ukaisamehe dhambi ya watu wako Israeli, na kuwarejeza tena katika nchi uliyowapa wao na baba zao. 26 Ikiwa mbingu zimefungwa, hata hakuna mvua, kwa sababu wamekukosa wewe; kama wakiomba wakikabili mahali hapa, na kulikiri jina lako, na kuiacha dhambi yao, uwatesapo; 27 basi usikie huko mbinguni, ukaisamehe dhambi ya watumwa wako, na ya watu wako Israeli; uwafundishapo njia njema iwapasayo waiendee; ukainyeshee mvua nchi yako, uliyowapa watu wako iwe urithi. 28 Ikiwa nchi imeingia njaa, au tauni, au ukosefu wa mvua, au ukungu, au nzige, au panzi; ikiwa adui wamewahusuru katika nchi ya miji yao, au ukiwapo msiba wo wote, au uele wo wote; 29 yo yote atakayoyaomba na kusihi mtu awaye yote, au watu wako Israeli wote pamoja, watakaojua kila mtu pigo lake mwenyewe, na msiba wake mwenyewe, akiinyoshea mikono nyumba hii; 30 basi usikie huko mbinguni, ukaapo, ukasamehe, ukampatilize kila mtu kwa kadiri ya njia zake zote; wewe umjuaye moyo; (maana wewe peke yako ndiwe uijuaye mioyo ya wanadamu); 31 ili wakuche wewe, waziendee njia zako, siku zote watakazoishi katika nchi uliyowapa baba zetu. 32 Hata na mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako kuu, na mkono wako ulio hodari, na mkono wako ulionyoshwa; hao watakapokuja na kuomba wakiielekea nyumba hii; 33 basi usikie huko mbinguni, toka makaoni mwako, ukatende yote atakayokuomba huyo mgeni; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukucha wewe, kama watu wako Israeli, tena wajue ya kuwa nyumba hii niliyoijenga imeitwa kwa jina lako. 34 Ikiwa watu wako wametoka kupigana na adui zao, utakakowatuma ko kote, wakikuomba kuuelekea mji huu uliouchagua, na nyumba hii niliyoijenga kwa jina lako; 35 basi uyasikie huko mbinguni wayaombayo, na kusihi, ukaitetee haki yao. 36 Wakikukosa, (maana hakuna mtu asiyekosa), hata uwakasirikie, na kuwatia mikononi mwa adui zao, wawahamishe, na kuwachukua mateka mpaka nchi iliyo mbali au iliyo karibu; 37 basi wakikumbuka katika nchi walikohamishwa, na kutubu, na kukusihi katika nchi ya uhamisho wao, wakisema, Tumekosa, tumetenda kwa ukaidi, tumefanya maovu; 38 wakurudiapo kwa mioyo yao yote, na kwa nia zao zote, katika nchi ya uhamisho wao, adui walikowahamisha, wakiomba na kuielekea nchi uliyowapa baba zao, na mji huu uliouchagua, na nyumba hii niliyoijenga kwa jina lako; 39 basi uyasikie toka mbinguni, toka makaoni mwako, wayaombayo, na kusihi, ukaitetee haki yao; ukawasamehe watu wako, waliokosa juu yako. 40 Na sasa, Ee Mungu wangu, macho yako yafumbuke, nakusihi, masikio yako yakasikilize maombi yaombwayo mahali hapa. 41 Sasa, Ee Bwana, Mungu, uondoke, uende kwenye raha yako, wewe na sanduku la nguvu zako; makuhani wako, Ee Bwana, Mungu, wavikwe wokovu, watakatifu wako na washangilie mema. 42 Ee Bwana, Mungu, usiurudishe nyuma uso wa masihi wako,uzikumbuke fadhili za Daudi mtumishi wako.

2 Mambo ya Nyakati 7

1 Basi Sulemani alipokwisha maombi hayo, moto ukashuka kutoka mbinguni, ukateketeza sadaka ya kuteketezwa na dhabihu; utukufu wa Bwana ukaijaza nyumba. 2 Wala makuhani hawakuweza kuingia nyumbani mwa Bwana, kwa kuwa utukufu wa Bwana umeijaza nyumba ya Bwana. 3 Wakatazama wana wa Israeli wote, uliposhuka ule moto, utukufu wa Bwana ulipokuwapo juu ya nyumba; wakasujudu kifulifuli hata nchi sakafuni, wakaabudu, wakamshukuru Bwana, wakisema, Kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele. 4 Ndipo mfalme na watu wote wakatoa dhabihu mbele za Bwana. 5 Mfalme Sulemani akatoa sadaka ya ng'ombe ishirini na mbili elfu, na kondoo mia na ishirini elfu. Ndivyo mfalme na watu wote walivyoifanya wakfu nyumba ya Mungu. 6 Wakasimama makuhani sawasawa na malinzi yao; Walawi nao pamoja na vinanda vya Bwana, alivyovifanya Daudi mfalme, ili kumshukuru Bwana, kwa maana fadhili zake ni za milele, hapo aliposifu Daudi kwa mikono yao; nao makuhani wakapiga panda mbele yao; nao Israeli wote wakasimama. 7 Tena Sulemani akaitakasa behewa katikati, iliyokuwa mbele ya nyumba ya Bwana; kwa kuwa hapo ndipo alipotoa sadaka za kuteketezwa, na mafuta ya sadaka za amani; kwa sababu ile madhabahu ya shaba aliyoifanya Sulemani haikutosha kuzipokea sadaka ya kuteketezwa, na sadaka ya unga, na mafuta. 8 Basi, wakati ule Sulemani akafanya sikukuu, na Israeli wote pamoja naye, kusanyiko kubwa sana, toka maingilio ya Hamathi mpaka kijito cha Misri, muda wa siku saba. 9 Hata siku ya nane wakaita kusanyiko la makini; kwa maana walishika kuitakasa madhabahu siku saba, na sikukuu siku saba. 10 Akawaruhusu watu waende hemani kwao siku ya ishirini na tatu, ya mwezi wa saba, wakifurahi na kuchangamka mioyoni kwa wema wote Bwana aliomfanyia Daudi, na Sulemani, na Israeli watu wake. 11 Hivyo Sulemani akaimaliza nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme; na yote yaliyomwingia Sulemani moyoni ayafanye nyumbani mwa Bwana, na nyumbani mwake mwenyewe, akayafanikisha. 12 Bwana akamtokea Sulemani usiku, akamwambia, Nimesikia uliyoyaomba, na mahali hapa nimejichagulia kuwa nyumba ya dhabihu. 13 Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi, au nikiwapelekea watu wangu tauni; 14 ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao. 15 Sasa macho yangu yatafumbuka, na masikio yangu yatasikiliza maombi ya watu waombao mahali hapa. 16 Maana sasa nimeichagua nyumba hii na kuitakasa, ili kwamba jina langu lipate kuwako huko milele; yatakuwako na macho yangu, na moyo wangu daima. 17 Nawe, ukienda mbele yangu kama alivyokwenda Daudi baba yako, ufanye sawasawa na yote niliyokuamuru, na kuzishika sheria zangu na hukumu zangu; 18 ndipo nitakithibitisha kiti cha enzi cha ufalme wako, kama nilivyoagana na Daudi baba yako, nikisema, Hutakosa kuwa na mtu wa kutawala katika Israeli. 19 Lakini mkigeuka, na kuziacha sheria zangu na amri zangu nilizoweka mbele yenu, mkienda, na kuitumikia miungu mingine, na kuiabudu; 20 ndipo nitawang'oa katika nchi yangu niliyowapa; na nyumba hii niliyoitakasa kwa jina langu, nitaiondosha itoke mbele zangu, nami nitaifanya kuwa mithali na tukano katikati ya watu wote. 21 Na nyumba hii, iliyo juu, kila apitaye ataona ushangao, atasema, Mbona Bwana ameitendea hivi nchi hii, na nyumba hii? 22 Nao watajibu, Kwa sababu walimwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka nchi ya Misri, wakashikamana na miungu mingine, wakaiabudu, na kuitumikia; kwa hiyo ameyaleta mabaya haya yote juu yao.

2 Mambo ya Nyakati 8

1 Ikawa miaka ishirini ilipopita, ambayo katika hiyo Sulemani aliijenga nyumba ya Bwana, na nyumba yake mwenyewe; 2 ndipo Sulemani akaijenga miji ile Hiramu aliyompa Sulemani, akawakalisha humo wana wa Israeli. 3 Naye Sulemani akaenda Hamath-zoba, akaushinda. 4 Akaujenga Tadmori wa nyikani, na miji yote ya hazina, aliyoijenga katika Hamathi. 5 Tena akaujenga Beth-horoni wa juu, na Beth-horoni wa chini, miji yenye boma, yenye kuta, na malango, na makomeo; 6 na Baalathi, na miji yote ya hazina Sulemani aliyokuwa nayo, na miji yote ya magari yake, na miji ya wapanda farasi wake, na ya anasa yote aliyopenda Sulemani kujenga humo Yerusalemu, na katika Lebanoni, na katika nchi yote ya mamlaka yake. 7 Basi kwa habari ya watu wote waliosalia wa Wahiti, na wa Waamori, na wa Waperizi, na wa Wahivi, na wa Wayebusi, wasiokuwa wa Israeli; 8 wa watoto wao waliosalia baada yao katika nchi, ambao wana wa Israeli hawakuwakomesha, katika hao Sulemani akawatumikisha shokoa hata leo. 9 Wala katika wana wa Israeli Sulemani hakuwafanya watumwa kazini mwake; lakini hao walikuwa watu wa vita, na wakuu wa majemadari wake, na maakida wa magari yake na wa wapanda farasi wake. 10 Na hao walikuwa maakida wakuu wa Sulemani, watu mia mbili na hamsini, waliotawala juu ya watu. 11 Sulemani akamleta binti Farao kutoka mji wa Daudi mpaka nyumba aliyomjengea; kwa kuwa alisema, Mke wangu hatakaa nyumbani mwa Daudi mfalme wa Israeli, kwa kuwa ni patakatifu, mahali palipofika sanduku la Bwana. 12 Ndipo Sulemani akamtolea Bwana sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu ya Bwana, aliyoijenga mbele ya ukumbi, 13 kadiri ilivyohitajiwa huduma ya kila siku, akitoa sawasawa na amri ya Musa, siku za sabato, na za mwezi mpya, na za sikukuu zilizoamriwa, mara tatu kila mwaka, yaani, sikukuu ya mikate isiyochachwa, na sikukuu ya majuma, na sikukuu ya vibanda. 14 Akaziamuru, sawasawa na agizo la Daudi babaye, zamu za makuhani za kutumika, nao Walawi kwa kadiri ya malinzi yao, ili kusifu, na kuhudumu mbele ya makuhani, kama ilivyohitajiwa kila siku; tena mabawabu kwa zamu zao za kila mlango; maana ndivyo alivyoamuru Daudi mtu wa Mungu. 15 Wala hawakuyaacha maagizo ya mfalme aliyowaamuru makuhani na Walawi kwa neno lo lote, wala kwa habari ya hazina. 16 Basi ikatengenezwa kazi yote ya Sulemani hata siku ya kutiwa msingi wa nyumba ya Bwana, na hata ilipokwisha. Hivyo ikamalizika nyumba ya Bwana. 17 Ndipo Sulemani akaenda Esion-geberi, na Elothi, pwani ya nchi ya Edomu. 18 Naye Hiramu akamletea merikebu kwa mikono ya watumishi wake, na watumishi waliokuwa wana-maji; nao wakafika Ofiri pamoja na watumishi wa Sulemani, wakachukua kutoka huko talanta mia nne na hamsini za dhahabu, wakamletea mfalme Sulemani.

2 Mambo ya Nyakati 9

1 Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani, alikuja ili amjaribu Sulemani kwa maswali ya fumbo huko Yerusalemu, mwenye wafuasi wengi, na ngamia wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia Sulemani, akamwambia mambo yote aliyokuwa nayo moyoni mwake. 2 Naye Sulemani akamfumbulia maswali yake yote; wala halikuwako neno alilofichiwa Sulemani, asimwambie. 3 Naye malkia wa Sheba alipoona hekima ya Sulemani, na nyumba aliyoijenga, 4 na vyakula vya mezani mwake, na kikao cha watumishi wake, na usimamizi wao wangoje wake, na mavazi yao; na wanyweshaji wake, na mavazi yao; na daraja yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana; roho yake ilizimia. 5 Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. 6 Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe umezidi kuliko habari nilizozisikia. 7 Heri watu wako, na heri hawa watumishi wako, wasimamao mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako. 8 Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa mfalme wake Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli, kuwathibitisha milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu na haki. 9 Basi akampa mfalme talanta mia na ishirini za dhahabu, na manukato mengi mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja wingi wa manukato, kama hayo aliyopewa mfalme Sulemani na malkia wa Sheba. 10 Tena watumishi wa Hiramu, pamoja na watumishi wa Sulemani, walioleta dhahabu kutoka Ofiri, wakaleta miti ya msandali, na vito vya thamani. 11 Mfalme akayafanya kwa miti hiyo ya msandali madari ya nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala haijatokea kama hiyo katika nchi ya Yuda. 12 Mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila alilotaka, zaidi ya vile alivyomletea mfalme. Basi akarudi, akaenda zake katika nchi yake, yeye na watumishi wake. 13 Basi uzani wa dhahabu iliyomfikia Sulemani mwaka mmoja, ndio talanta mia sita sitini na sita za dhahabu; 14 mbali na ile waliyoileta wachuuzi na wafanya biashara; tena wafalme wote wa Arabuni, na maliwali wa nchi wakamletea Sulemani dhahabu na fedha. 15 Mfalme Sulemani akafanya ngao mia mbili za dhahabu iliyofuliwa; ngao moja hupata shekeli mia sita za dhahabu iliyofuliwa. 16 Na vigao mia tatu vya dhahabu iliyofuliwa; kigao kimoja hupata shekeli mia tatu za dhahabu; mfalme akaviweka katika nyumba ya mwitu wa Lebanoni. 17 Tena mfalme akafanya kiti cha enzi kikubwa cha pembe, akakifunikiza kwa dhahabu iliyo safi. 18 Kiti kile kilikuwa na daraja sita, tena na kikao cha miguu cha dhahabu, navyo vilikuwa vimeshikamana na kiti; na mikono huko na huko mahali pa kuketi, na simba wawili wakisimama kando ya hiyo mikono. 19 Na simba kumi na wawili wamesimama juu ya daraja sita, huko na huko; wala hakikufanyika kwa mfano wake katika ufalme wo wote. 20 Na vyombo vyote vya kunywea vya mfalme Sulemani vilikuwa vya dhahabu, na vyombo vyote vya nyumba ya mwitu wa Lebanoni vilikuwa vya dhahabu iliyosafika; fedha haikuhesabiwa kuwa kitu siku za Sulemani. 21 Kwa kuwa mfalme alikuwa na merikebu zilizokwenda Tarshishi pamoja na watumishi wa Hiramu; mara moja katika miaka mitatu huja merikebu za Tarshishi, zikileta dhahabu, na fedha, na pembe, na nyani, na tausi. 22 Basi mfalme Sulemani akawapita wafalme wote wa duniani kwa mali, na kwa hekima. 23 Wafalme wote wa duniani wakamtafuta Sulemani uso wake, ili waisikie hekima yake, Mungu aliyomtia moyoni. 24 Wakaleta kila mtu zawadi yake, vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na mavazi, na silaha, na manukato, na farasi, na nyumbu, hesabu yake ya mwaka kwa mwaka. 25 Sulemani akawa na mazizi ya farasi na magari elfu nne, na wapandao farasi kumi na mbili elfu, aliowaweka katika miji ya magari, na pamoja na mfalme huko Yerusalemu. 26 Akatawala juu ya wafalme wote toka Mto hata nchi ya Wafilisti, na hata mpaka wa Misri. 27 Mfalme akafanya fedha humo Yerusalemu kuwa kama mawe, na mierezi akaifanya kuwa kama mikuyu iliyomo Shefela, kwa kuwa mingi. 28 Wakamletea Sulemani farasi kutoka Misri, na kutoka nchi zote. 29 Basi mambo yake Sulemani yaliyosalia, ya kwanza, na ya mwisho, je! Hayakuandikwa katika tarehe ya Nathani nabii, katika unabii wa Ahiya, Mshiloni, na katika maono ya Ido mwonaji juu ya Yeroboamu mwana wa Nebati? 30 Akatawala Sulemani katika Yerusalemu juu ya Israeli wote miaka arobaini. 31 Naye Sulemani akalala na baba zake, akazikwa mjini mwa Daudi babaye; akatawala Rehoboamu mwanawe badala yake.

2 Mambo ya Nyakati 10

1 Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekuja Shekemu, ili wamfanye mfalme. 2 Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati aliposikia, (maana alikuwako Misri, ambako amekimbilia mbele ya mfalme Sulemani), Yeroboamu akarudi kutoka Misri. 3 Wakapeleka ujumbe, wakamwita, Yeroboamu akaja na Israeli wote, wakamwambia Rehoboamu, wakasema, 4 Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa upunguze utumwa mgumu wa baba yako, na kongwa lake zito alilotutwika, nasi tutakutumikia. 5 Akawaambia, Mnirudie baada ya siku tatu. Watu wakaenda zao. 6 Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee, waliosimama mbele ya Sulemani baba yake, alipokuwa hai bado, akasema, Mwanipa shauri gani la kuwajibu watu hawa? 7 Wakamwambia, wakasema, Ukiwa mwema kwao watu hawa, na kuwapendeza, na kuwaambia maneno mazuri, ndipo watakapokuwa watumishi wako siku zote. 8 Lakini akaliacha shauri lile la wazee walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, waliosimama mbele yake. 9 Akawaambia, Je! Mwanipa shauri gani la kuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakisema, Utufanyie jepesi kongwa alilotutwika baba yako. 10 Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliosema nawe, wakinena, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, lakini wewe tufanyie jepesi; uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. 11 Basi kama baba yangu aliwatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu akiwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa nge. 12 Basi Yeroboamu na watu wote wakamjia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu. 13 Mfalme akawajibu kwa ukali; mfalme Rehoboamu akaliacha shauri la wazee, akasema nao kwa shauri la vijana, 14 akinena, Baba yangu aliwafanyia kongwa zito, nami nitawaongezea; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa nge. 15 Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Mungu, ili alithibitishe neno lake alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa mkono wa Ahiya Mshiloni. 16 Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hawasikilizi, watu wakamjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese; nendeni zenu hemani kwenu, enyi Israeli, kila mtu; sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Daudi. Basi wakaenda zao Israeli wote hemani kwao. 17 Lakini kwa habari za wana wa Israeli waliokaa katika miji ya Yuda, Rehoboamu alitawala juu yao. 18 Ndipo mfalme Rehoboamu akamtuma Adoramu, msimamizi wa shokoa; nao wana wa Israeli wakamtupia mawe, hata akafa. Mfalme Rehoboamu akafanya haraka kupanda garini mwake, ili akimbilie Yerusalemu. 19 Hivyo Israeli wakaasi juu ya nyumba ya Daudi, hata leo.

2 Mambo ya Nyakati 11

1 Hata Rehoboamu alipofika Yerusalemu, akakusanya nyumba ya Yuda na Benyamini, watu wateule mia na themanini elfu waliokuwa hodari, watu wa vita, ili wapigane juu ya Israeli, ili wamrudishie Rehoboamu huo ufalme. 2 Lakini neno la Bwana likamjia Shemaya mtu wa Mungu, kusema, 3 Mwambie Rehoboamu mwana wa Sulemani, mfalme wa Yuda, uwaambie na Israeli wote waliomo Yuda na Benyamini, ukisema, 4 Bwana asema hivi, Hamtapanda wala kupigana na ndugu zenu; rudini kila mtu nyumbani kwake; kwa kuwa jambo hili limetoka kwangu. Basi, wakayasikiliza maneno ya Bwana, wakarudi katika kumwendea Yeroboamu. 5 Naye Rehoboamu akakaa Yerusalemu, akajenga miji yenye ngome katika Yuda. 6 Akajenga na Bethlehemu, na Etamu, na Tekoa, 7 na Bethsuri, na Soko, na Adulamu, 8 na Gathi, na Maresha, na Zifu, 9 na Adoraimu, na Lakishi, na Azeka, 10 na Sora, na Aiyaloni, na Hebroni, iliyoko katika Yuda na Benyamini, miji yenye maboma. 11 Akazifanya imara hizo ngome, akaweka majemadari humo, na akiba ya vyakula, na mafuta, na mvinyo. 12 Na ndani ya miji yote mmoja mmoja aliweka ngao na mikuki, akaifanya kuwa na nguvu nyingi mno. Yuda na Benyamini ikawa milki yake. 13 Wakamwendea makuhani na Walawi waliokuwa katika Israeli yote, kutoka mpaka wao wote. 14 Kwani Walawi wakaacha malisho yao, na milki yao, wakaja Yuda na Yerusalemu; kwa sababu Yeroboamu na wanawe waliwatupa, ili wasimfanyie Bwana ukuhani; 15 naye akajiwekea makuhani wa mahali pa juu, na wa wale majini, na wa zile ndama alizozifanya. 16 Na kutoka katika kabila zote za Israeli, wakaandamwa na hao waliojikaza nia kumtafuta Bwana, Mungu wa Israeli, wakaja Yerusalemu, ili wamtolee dhabihu Bwana, Mungu wa baba zao. 17 Hivyo wakaufanya imara kwa miaka mitatu ufalme wa Yuda, na kumtia nguvu Rehoboamu mwana wa Sulemani; kwa maana muda wa miaka mitatu wakaiendea njia ya Daudi na Sulemani. 18 Rehoboamu akaoa mke, Mahalathi binti Yerimothi mwana wa Daudi, na wa Abihaili binti Eliabu, mwana wa Yese; 19 akamzalia wana, Yeushi, na Shemaria, na Zahamu. 20 Kisha baada yake akamwoa Maaka, binti Absalomu; na yeye akamzalia Abiya, na Atai, na Ziza, na Shelomithi. 21 Rehoboamu akampenda Maaka binti Absalomu kuliko wakeze wote na masuria yake; (maana alioa wake kumi na wanane, na masuria sitini, akazaa wana ishirini na wanane na binti sitini). 22 Rehoboamu akamsimamisha Abiya, mwana wa Maaka, kuwa mkuu, mtawala kati ya nduguze, kwa kuwa aliazimia kumtawaza awe mfalme. 23 Akafanya kwa akili, akawatawanya wanawe wote kati ya nchi zote za Yuda na Benyamini, katika kila mji wenye boma; akawapa vyakula tele. Akawatafutia wake wengi.

2 Mambo ya Nyakati 12

1 Ikawa ulipothibitika ufalme wa Rehoboamu, naye amepata nguvu, aliiacha torati ya Bwana, na Israeli wote pamoja naye. 2 Ikawa katika mwaka wa tano wa mfalme Rehoboamu, akapanda Shishaki, mfalme wa Misri, juu ya Yerusalemu; kwa kuwa walikuwa wamemwasi Bwana; 3 mwenye magari elfu moja na mia mbili, na wapanda farasi sitini elfu; na watu wasiohesabika, waliotoka Misri pamoja naye; Walubi, na Wasukii, na Wakushi. 4 Akaitwaa miji yenye maboma iliyokuwa ya Yuda, akaja Yerusalemu. 5 Ndipo akaja Shemaya nabii kwa Rehoboamu, na kwa wakuu wa Yuda, waliokusanyika Yerusalemu kwa sababu ya Shishaki, akawaambia, Bwana asema hivi, Ninyi mmeniacha mimi, kwa hiyo nami nimewaacha ninyi mkononi mwa Shishaki. 6 Ndipo wakajinyenyekeza wakuu wa Israeli na mfalme; wakasema, Bwana ndiye mwenye haki. 7 Naye Bwana alipoona ya kwamba wamejinyenyekeza, neno la Bwana likamjia Shemaya, kusema, Wamejinyenyekeza; sitawaharibu; lakini nitawapa wokovu punde, wala ghadhabu yangu haitamwagika juu ya Yerusalemu kwa mkono wa Shishaki. 8 Walakini watamtumikia; ili wapate kujua utumwa wangu, na huo utumwa wa falme za nchi. 9 Basi Shishaki, mfalme wa Misri, akapanda juu ya Yerusalemu, akazichukua hazina za nyumba ya Bwana, na hazina za nyumba ya mfalme; akazichukua zote. Akazichukua pia ngao za dhahabu alizozifanya Sulemani. 10 Mfalme Rehoboamu akafanya ngao za shaba mahali pake, akawakabidhi wakuu wa walinzi, waliongoja mlangoni pa nyumba ya mfalme. 11Ikawa kila wakati mfalme alipoingia nyumbani mwa Bwana, wakaja walinzi wakazichukua, wakazirudisha tena chumbani mwa walinzi. 12 Naye alipojinyenyekeza, ghadhabu ya Bwana ikamgeukia mbali, asimharibu kabisa; tena yalionekana katika Yuda mambo mema. 13 Basi mfalme Rehoboamu akajitia nguvu katika Yerusalemu, akatawala; maana Rehoboamu alikuwa na umri wa miaka arobaini na mmoja alipoanza kutawala, akatawala miaka kumi na saba huko Yerusalemu, mji aliouchagua Bwana miongoni mwa kabila zote za Israeli, ili aliweke huko jina lake. Na jina la mamaye aliitwa Naama Mwamoni. 14 Naye akatenda yaliyo maovu, kwa kuwa hakuukaza moyo wake amtafute Bwana. 15 Basi mambo yake Rehoboamu, ya kwanza na ya mwisho, je! Hayakuandikwa katika tarehe za Shemaya nabii na Ido mwonaji, kwa jinsi ya kuandika nasaba? Kulikuwa na vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu siku zote. 16 Rehoboamu akalala na babaze, akazikwa katika mji wa Daudi. Na Abiya mwanawe alitawala mahali pake.

2 Mambo ya Nyakati 13

1 Katika mwaka wa kumi na nane wa mfalme Yeroboamu, akaanza Abiya kutawala juu ya Yuda. 2 Miaka mitatu akatawala huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Maaka binti Urieli wa Gibea. Kulikuwa na vita kati ya Abiya na Yeroboamu. 3 Abiya akapanga vita mwenye jeshi la watu hodari wa vita, watu wateule mia nne elfu; naye Yeroboamu akapanga vita juu yake mwenye watu wateule mia nane elfu, waliokuwa waume mashujaa. 4 Basi Abiya akasimama juu ya kilima cha Semaraimu, kilichoko milimani mwa Efraimu, akasema, Nisikieni, enyi Yeroboamu na Israeli wote; 5 je! Haikuwapasa kujua ya kwamba Bwana, Mungu wa Israeli, alimpa Daudi ufalme juu ya Israeli milele, yeye na wanawe kwa agano la chumvi? 6 Lakini Yeroboamu mwana wa Nebati, mtumwa wa Sulemani mwana wa Daudi, akainuka, akamfanyia fitina bwana wake. 7 Wakamkusanyikia watu mabaradhuli, wasiofaa kitu, waliojitia nguvu juu ya Rehoboamu mwana wa Sulemani, Rehoboamu alipokuwa kijana na wa moyo mwororo, asiweze kuwazuia. 8 Hata sasa mwajidhania kuwa mtauzuia ufalme wa Bwana mikononi mwa wana wa Daudi; nanyi mmekuwa jamii kubwa, na kwenu mna ndama za dhahabu alizowafanyia Yeroboamu kuwa miungu. 9 Je! Hamkuwafukuza makuhani wa Bwana, wana wa Haruni, na Walawi; mkajifanyia makuhani kama wafanyavyo watu wa nchi nyingine? Hata ye yote ajaye kujifanya wakfu na ndama, na kondoo waume saba, aweza kuwa kuhani wa hiyo isiyo miungu. 10 Lakini sisi, Bwana ndiye Mungu wetu, wala sisi hatukumwacha; tena tunao makuhani wanaomtumikia Bwana, wana wa Haruni, na Walawi, kwa kazi yao; 11 nao humtolea Bwana kila asubuhi, na kila jioni, sadaka za kuteketezwa na fukizo la manukato; mikate ya wonyesho pia huiweka kwa taratibu yake juu ya meza takatifu, na kinara cha dhahabu chenye taa zake, kuwaka kila jioni; kwa maana sisi twayalinda malinzi ya Bwana, Mungu wetu; bali ninyi mmemwacha. 12 Na tazama, Mungu yu pamoja nasi atutangulie, na makuhani wake wenye mapanda, ili wapige sauti ya kugutusha juu yenu. Enyi wana wa Israeli, msipigane na Bwana, Mungu wa baba zenu; kwani hamtafanikiwa. 13 Lakini Yeroboamu aliwazungushia waviziao kwa nyuma; basi wao wakawa mbele ya Yuda, na wale waviziao nyuma yao. 14 Na Yuda walipotazama nyuma, angalia, vita vikawa mbele na nyuma; wakamlilia Bwana, na makuhani wakapiga mapanda. 15 Ndipo wakapiga kelele watu wa Yuda; ikawa, watu na Yuda walipopiga kelele, Mungu akampiga Yeroboamu na Israeli wote mbele ya Abiya na Yuda. 16 Wana wa Israeli wakakimbia mbele ya Yuda; naye Mungu akawaua mikononi mwao. 17 Abiya na watu wake wakawapiga mapigo makuu; hata wakaanguka wameuawa wa Israeli mia tano elfu, watu wateule. 18 Ndivyo walivyotiishwa wana wa Israeli wakati ule, wakashinda wana wa Yuda, kwa kuwa walimtegemea Bwana, Mungu wa baba zao. 19 Abiya akamfuata Yeroboamu, akamnyang'anya miji, Betheli na miji yake, na Yeshana na miji yake, na Efroni na miji yake. 20 Wala Yeroboamu hakupata nguvu tena siku za Abiya; kisha Bwana akampiga, akafa. 21 Ila Abiya akapata nguvu, akaoa wake kumi na wanne, akazaa wana ishirini na wawili, na binti kumi na sita. 22 Na mambo ya Abiya yaliyosalia, na njia zake, na maneno yake, yameandikwa katika kitabu cha maelezo cha nabii Ido.

2 Mambo ya Nyakati 14

1 Basi Abiya akalala na baba zake, wakamzika mjini mwa Daudi, akatawala Asa mwanawe mahali pake; katika siku zake nchi ikastarehe miaka kumi. 2 Basi, Asa akafanya yaliyo mema, yaliyo ya adili, machoni pa Bwana, Mungu wake; 3 maana aliziondoa madhabahu za kigeni, na mahali pa juu, akazivunja nguzo, akayakata-kata maashera; 4 akawaamuru Yuda wamtafute Bwana, Mungu wa baba zao, na kuzitenda torati na amri. 5 Tena akaondoa kutoka miji yote ya Yuda mahali pa juu na sanamu za jua; ufalme ukastarehe mbele yake. 6 Akajenga miji yenye maboma katika Yuda; kwa kuwa nchi ilikuwa imestarehe, wala hakuwa na vita miaka ile; kwa sababu Bwana amemstarehesha. 7 Naye akawaambia Yuda, Na tuijenge miji hii, na kuizungushia maboma, na minara, na malango, na makomeo; nchi bado ikalipo mbele yetu, kwa kuwa tumemtafuta Bwana, Mungu wetu; naam, tumemtafuta, naye amemstarehesha pande zote. Basi wakajenga, wakafanikiwa. 8 Naye Asa alikuwa na jeshi waliochukua ngao na mikuki, katika Yuda mia tatu elfu; na katika Benyamini wenye kuchukua vigao na kupinda upinde, mia mbili na themanini elfu; hao wote walikuwa mashujaa. 9 Kisha, akatoka juu yao Zera Mkushi, mwenye jeshi elfu elfu, na magari mia tatu; akaja Maresha. 10 Akatoka Asa amlaki, wakapanga vita Maresha bondeni mwa Sefatha. 11 Naye Asa akamlilia Bwana, Mungu wake, akasema, Bwana, hapana kuliko wewe aliye wa kusaidia, kati yake yeye aliye hodari, na yeye asiye na nguvu; utusaidie, Ee Bwana, Mungu wetu; kwa kuwa sisi twakutegemea wewe, na kwa jina lako tumekuja juu ya jamii kubwa hii. Ee Bwana, wewe ndiwe Mungu wetu, asikushinde mwanadamu. 12 Basi, Bwana akawapiga Wakushi mbele ya Asa, na mbele ya Yuda; na Wakushi wakakimbia. 13 Asa na watu waliokuwa pamoja naye wakawafuata mpaka Gerari; nao wengi wakaanguka wa Wakushi hata wasiweze kupona; kwa sababu waliangamizwa mbele za Bwana, na mbele ya jeshi lake; na hao wakachukua mateka mengi sana. 14 Wakaipiga miji yote kando-kando ya Gerari; maana hofu ya Bwana ikawajia; nao wakaiteka nyara miji yote, kwa maana zilikuwamo ndani yake nyara nyingi mno. 15 Wakazipiga pia hema za ng'ombe, wakachukua kondoo wengi na ngamia, wakarudi Yerusalemu.

2 Mambo ya Nyakati 15

1 Ndipo roho ya Mungu ikamjia Azaria mwana wa Odedi; 2 naye akatoka ili amlaki Asa, akamwambia, Nisikieni, Ee Asa, na Yuda wote na Benyamini; Bwana yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye; nanyi mkimtafuta ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi. 3 Basi tangu siku nyingi Israeli wamekuwa hawana Mungu wa kweli, wala hawana kuhani afundishaye, wala hawana torati; 4 lakini walipomgeukia Bwana, Mungu wa Israeli, katika msiba wao, na kumtafuta, akaonekana kwao. 5 Hata na zamani zile hakukuwa na amani kwake atokaye, wala kwake aingiaye, ila fadhaa kubwa juu yao wote wakaao katika nchi. 6 Wakavunjika-vunjika, taifa juu ya taifa, na mji juu ya mji; kwani Mungu aliwafadhaisha kwa shida zote. 7 Nanyi jipeni nguvu, wala mikono yenu isilegee; kwa maana kazi yenu itakuwa na ijara. 8 Naye Asa alipoyasikia maneno hayo, yaani, unabii wa mwana wa Odedi nabii, akatiwa nguvu, akayaondolea mbali machukizo yote katika nchi ya Yuda na Benyamini, na katika miji aliyoitwaa milimani mwa Efraimu; akaifanyiza tena madhabahu ya Bwana, iliyokuwako mbele ya ukumbi wa Bwana. 9 Akakusanya Yuda wote na Benyamini, na hao wageni waliokaa kwao, wa Efraimu, na wa Manase, na wa Simeoni; kwa kuwa walimwangukia wengi katika Israeli, walipoona kwamba Bwana, Mungu wake, alikuwa pamoja naye. 10 Basi wakakusanyika huko Yerusalemu mwezi wa tatu, katika mwaka wa kumi na tano wa kumiliki kwake Asa. 11 Wakamchinjia Bwana siku ile, katika nyara walizozileta, dhabihu za ng'ombe mia saba, na kondoo elfu saba. 12 Wakafanya agano, ya kuwa watamtafuta Bwana, Mungu wa baba zao, kwa mioyo yao yote, na kwa roho zao zote; 13 na ya kwamba ye yote asiyemtafuta Bwana, Mungu wa Israeli, atauawa, akiwa mdogo au mkubwa, kwamba ni mwanamume au mwanamke. 14 Wakamwapia Bwana kwa sauti kuu, na kwa kelele, na kwa mapanda, na kwa baragumu. 15 Na Yuda wote wakakifurahia kile kiapo; kwani wameapa kwa moyo wao wote, na kumtafuta kwa mapenzi yao pia; naye ameonekana kwao; naye Bwana akawastarehesha pande zote. 16 Hata na Maaka mamaye Asa, mfalme akamwondolea daraja yake asiwe malkia, kwa kuwa amefanya sanamu ya kuchukiza kwa Ashera; basi Asa akaikata sanamu yake, akaiponda, akaiteketeza penye kijito cha Kidroni. 17 Lakini mahali pa juu hapakuondolewa katika Israeli; ila moyo wake Asa ulikuwa mkamilifu siku zake zote. 18 Akavileta nyumbani mwa Mungu vitu alivyovitakasa babaye, na vile alivyovitakasa mwenyewe, fedha, na dhahabu, na vyombo. 19 Wala hapakuwa na vita tena hata mwaka wa thelathini na tano wa kutawala kwake Asa.

2 Mambo ya Nyakati 16

1 Katika mwaka wa thelathini na sita wa kutawala kwake Asa, Baasha mfalme wa Israeli akapanda juu ya Yuda, akaujenga Rama, ili asimwache mtu ye yote kutoka wala kuingia kwa Asa mfalme wa Yuda. 2 Ndipo Asa akatoa fedha na dhahabu katika hazina za nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme, akampelekea Ben-hadadi mfalme wa Shamu, aliyekaa Dameski, akasema, 3 Kwangu na kwako na liwe agano kama lilivyokuwa kwa baba yangu na baba yako; angalia, nimekuletea fedha na dhahabu; basi, uvunje agano lako na Baasha, mfalme wa Israeli, ili aniondokee mimi. 4 Naye Ben-hadadi akamsikiliza mfalme Asa, akawapeleka maakida wa majeshi yake juu ya miji ya Israeli; wakapiga Iyoni, na Dani, na Abel-maimu, na miji ya hazina yote ya Naftali. 5 Ikawa Baasha aliposikia habari hiyo, akaacha kuujenga Rama, akaikomesha kazi yake. 6 Ndipo mfalme Asa akawatwaa Yuda wote; nao wakayachukua mawe ya Rama, na miti yake, aliyoijengea Baasha; naye akajenga kwa vitu hivyo Geba na Mispa. 7 Wakati ule Hanani mwonaji akamwendea Asa mfalme wa Yuda, akamwambia, Kwa kuwa umemtegemea mfalme wa Shamu, wala hukumtegemea Bwana, Mungu wako, kwa hiyo limeokoka jeshi la mfalme wa Shamu mkononi mwako. 8 Je! Hao Wakushi na Walubi hawakuwa jeshi kubwa mno, wenye magari na wapanda farasi wengi sana? Lakini, kwa kuwa ulimtegemea Bwana, aliwatia mkononi mwako. 9 Kwa maana macho ya Bwana hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake. Kwa hayo umetenda upumbavu; kwani tangu sasa utakuwa na vita. 10 Ndipo Asa akamkasirikia mwonaji, akamtia nyumbani mwa mkatale; maana amemghadhibikia kwa sababu ya neno hilo. Na Asa akawaonea baadhi ya watu wakati ule ule. 11 Na tazama, mambo yake Asa, ya kwanza na ya mwisho, angalia, yameandikwa katika kitabu cha wafalme wa Yuda na Israeli. 12 Akashikwa Asa na ugonjwa wa miguu katika mwaka wa thelathini na kenda wa kumiliki kwake; ugonjwa wake ukazidi sana; lakini hakumtafuta Bwana katika ugonjwa wake, bali waganga. 13 Asa akalala na babaze, akafa katika mwaka wa arobaini na mmoja wa kumiliki kwake. 14 Wakamzika katika makaburi yake mwenyewe, aliyojichimbia katika mji wa Daudi, wakamlaza juu ya kitanda kilichojazwa manukato, na kila namna ya machanganyiko ya hao mafundi wa dawa; wakamfukizia mafukizo makuu sana.

2 Mambo ya Nyakati 17

1 Na Yehoshafati mwanawe akatawala mahali pake, akajitia nguvu juu ya Israeli. 2 Akaweka jeshi katika miji yote yenye maboma ya Yuda, akatia na askari walinzi katika nchi ya Yuda, na katika miji ya Efraimu, aliyoitwaa Asa babaye. 3 Naye Bwana alikuwa pamoja na Yehoshafati, kwa kuwa alikwenda katika njia za kwanza za Daudi babaye, asiyatafute mabaali; 4 lakini alimtafuta Mungu wa baba yake, akaenda katika amri zake, wala si katika matendo ya Israeli. 5 Kwa hiyo Bwana akauthibitisha ufalme mkononi mwake; Yehoshafati akaletewa zawadi na Yuda wote; basi akawa na mali na heshima tele. 6 Ukainuliwa moyo wake katika njia za Bwana; na zaidi ya hayo akapaondoa mahali pa juu, na maashera, katika Yuda. 7 Tena, katika mwaka wa tatu wa kutawala kwake, akawatuma wakuu wake, yaani, Ben-haili, na Obadia, na Zekaria, na Nethaneli, na Mikaya, ili kufundisha mijini mwa Yuda; 8 na pamoja nao Walawi, yaani, Shemaya, na Nethania, na Zebadia, na Asaheli, na Shemiramothi, na Yehonathani, na Adonia, na Tobia, na Tob-adonia, Walawi; na pamoja nao Elishama na Yehoramu, makuhani. 9 Wakafundisha katika Yuda, wenye kitabu cha torati ya Bwana; wakazunguka katika miji yote ya Yuda, wakafundisha kati ya watu. 10 Hofu ya Bwana ikaziangukia falme za nchi zote zilizozunguka Yuda, wasipigane vita na Yehoshafati. 11 Na baadhi ya Wafilisti walimletea Yehoshafati zawadi, na fedha ya kodi; Waarabu nao wakamletea makundi, kondoo waume saba elfu na mia saba, na mabeberu saba elfu na mia saba. 12 Ukuu wake Yehoshafati ukazidi sana; akajenga katika Yuda ngome na miji ya hazina. 13 Naye alikuwa na kazi nyingi katika miji ya Yuda; na watu wa vita, watu mashujaa humo Yerusalemu. 14 Na hivi ndivyo walivyohesabiwa kwa mbari za baba zao; wa Yuda, maakida wa maelfu; Adna jemadari, na pamoja naye watu mashujaa mia tatu elfu; 15 na wa pili wake Yehohanani akida, na pamoja naye mia mbili na themanini elfu; 16 na baada yake Amasia mwana wa Zikri, aliyejitoa kwa Bwana kwa moyo, na pamoja naye mia mbili elfu, watu mashujaa; 17 na wa Benyamini; Eliada mtu shujaa, na pamoja naye mia mbili elfu wenye nyuta na ngao; 18 na wa pili wake Yehozabadi, na pamoja naye mia na themanini elfu waliojiweka tayari kwa vita. 19 Hao ndio waliomngojea mfalme, zaidi ya hao mfalme aliowaweka katika miji yenye maboma katika Yuda yote.

2 Mambo ya Nyakati 18

1 Basi, Yehoshafati alikuwa na mali na heshima tele, tena akafanya ujamaa na Ahabu. 2 Hata baada ya miaka kadha wa kadha akamshukia Ahabu huko Samaria. Ahabu akamchinjia kondoo na ng'ombe tele, yeye na watu waliokuwa pamoja naye, akamshawishi ili apande pamoja naye waende Ramoth-gileadi. 3 Ahabu, mfalme wa Israeli, akamwambia Yehoshafati, mfalme wa Yuda, Je! Utakwenda nami mpaka Ramoth-gileadi? Akamjibu, Mimi ni kama wewe, na watu wangu kama watu wako; nasi tutakuwa pamoja nawe vitani. 4 Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli, Uulize leo, nakusihi, kwa neno la Bwana. 5 Ndipo mfalme wa Israeli akawakusanya manabii, watu mia nne; akawaambia, Je! Tuende Ramoth-gileadi vitani, au niache? Wakasema, Kwea; kwa kuwa Mungu atautia mkononi mwa mfalme. 6 Lakini Yehoshafati akasema, Je! Hayupo hapa nabii wa Bwana tena, ili tumwulize yeye? 7 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Yupo mtu mmoja, ambaye tungeweza kumwuliza Bwana kwa yeye; lakini namchukia; kwa sababu hanibashirii mema kamwe, ila siku zote mabaya; naye ndiye Mikaya mwana wa Imla. Yehoshafati akasema, La! Mfalme asiseme hivi. 8 Ndipo mfalme wa Israeli akamwita akida mmoja, akasema, Mlete hima Mikaya mwana wa Imla. 9 Basi, mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wamekaa kila mtu katika kiti chake cha enzi, wamevaa mavazi yao, wakikaa penye sakafu pa kuingilia lango la Samaria; nao manabii wote wakafanya unabii mbele yao. 10 Na Zedekia mwana wa Kenaana akajifanyia pembe za chuma, akasema, Bwana asema hivi, Kwa hizi utawasukuma Washami, hata watakapoangamia. 11 Na manabii wote wakatoa unabii huo, wakisema, Kwea Ramoth-gileadi, ukafanikiwe, kwa kuwa Bwana atautia mkononi mwa mfalme. 12 Na yule mjumbe, aliyekwenda kumwita Mikaya, akamwambia, akasema, Angalia, maneno ya manabii kwa kinywa kimoja yasema mema kwa mfalme; neno lako basi na liwe kama mojawapo lao, ukaseme mema. 13 Mikaya akasema, Kama aishivyo Bwana, neno lile atakalolinena Mungu wangu, ndilo nitakalolinena. 14 Na alipokuja kwa mfalme, mfalme akamwambia, Je! Mikaya, tuende Ramoth-gileadi vitani, au niache? Akasema, Kweeni, mkafanikiwe; nao watatiwa mikononi mwenu. 15 Mfalme akamwambia, Mara ngapi nikuapishe, usiniambie neno ila yaliyo kweli, kwa jina la Bwana? 16 Akasema, Naliwaona Waisraeli wote wametawanyika milimani, kama kondoo wasio na mchungaji; Bwana akasema, Hawa hawana bwana; na warudi kila mtu nyumbani kwake kwa amani. 17 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Je! Sikukuambia, hatanibashiria mema, ila mabaya? 18 Mikaya akasema, Sikieni basi neno la Bwana; Nalimwona Bwana ameketi katika kiti chake cha enzi na jeshi lote la mbinguni wamesimama mkono wake wa kuume na wa kushoto. 19 Bwana akasema, Ni nani atakayemdanganya Ahabu mfalme wa Israeli, ili akwee Ramoth-gileadi akaanguke? Basi huyu akasema hivi; na huyu hivi. 20 Akatoka pepo, akasimama mbele za Bwana, akasema, Mimi nitamdanganya. Bwana akamwambia, Jinsi gani? 21 Akasema, Nitaondoka, na kuwa pepo wa uongo vinywani mwa manabii wake wote. Akasema, Utamdanganya, na kudiriki pia; ondoka, ukafanye hivyo. 22 Basi sasa, angalia, Bwana ametia pepo wa uongo vinywani mwa manabii wako hawa; naye Bwana amenena mabaya juu yako. 23 Ndipo akakaribia Zedekia mwana wa Kenaana, akampiga Mikaya kofi la shavu, akasema, Alitokaje kwangu roho ya Bwana ili aseme na wewe? 24 Mikaya akasema, Angalia utaona siku ile, utakapoingia katika chumba cha ndani ili ujifiche. 25 Mfalme wa Israeli akasema, Mchukueni Mikaya mkamrudishe kwa Amoni mkuu wa mji, na kwa Yoashi mwana wa mfalme; 26 mkaseme, Mfalme asema hivi, Mtieni huyu gerezani, mkamlishe chakula cha shida, na maji ya shida, hata nitakaporudi kwa amani. 27 Mikaya akasema, Ukirudi kabisa kwa amani, Bwana hakusema kwa mimi. Akasema, Sikieni, enyi watu wote. 28 Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda wakakwea mpaka Ramoth-gileadi. 29 Mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Nitajibadilisha, na kuingia vitani; lakini wewe uvae mavazi yako. Mfalme wa Israeli akajibadilisha; nao wakaingia vitani. 30 Basi mfalme wa Shamu alikuwa amewaamuru maakida wa magari yake, akisema, Msipigane na mdogo wala mkuu, ila na mfalme wa Israeli peke yake. 31 Ikawa maakida wa magari walipomwona Yehoshafati, wakasema, Mfalme wa Israeli ni huyu. Basi wakamgeukia ili wapigane naye; lakini Yehoshafati akalia, na Bwana akamsaidia; Mungu akawafarakisha kwake. 32 Ikawa, maakida wa magari walipoona ya kuwa siye mfalme wa Israeli, wakageuka nyuma wasimfuate. 33 Na mtu mmoja akavuta upinde kwa kubahatisha, akampiga mfalme wa Israeli mahali pa kuungana mavazi yake ya chuma; kwa hiyo akamwambia mwendesha gari, Geuza mkono wako, unichukue kutoka katika majeshi; kwa kuwa nimejeruhiwa sana. 34 Pigano likazidi siku ile; lakini mfalme wa Israeli akajitegemeza garini juu ya Washami hata jioni; akafa kama wakati wa kuchwa kwa jua.

2 Mambo ya Nyakati 19

1 Yehoshafati mfalme wa Yuda akarudi Yerusalemu nyumbani kwake kwa amani. 2 Yehu mwana wa Hanani mwonaji akatoka kwenda kumlaki, akamwambia mfalme Yehoshafati, Je! Imekupasa kuwasaidia waovu, na kuwapenda wamchukiao Bwana? Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa Bwana. 3 Walakini yameonekana mema ndani yako, kwa kuwa umeyaondoa maashera katika nchi, na moyo wako umeukaza kumtafuta Mungu. 4 Na Yehoshafati akakaa Yerusalemu; akatoka tena kwenda kati ya watu toka Beer-sheba mpaka milima ya Efraimu, akawarudisha kwa Bwana, Mungu wa baba zao. 5 Akasimamisha makadhi katika nchi, katikati ya miji yote yenye maboma ya Yuda, mji kwa mji; 6 akawaambia hao makadhi, Angalieni myafanyayo; kwa kuwa hammfanyii mwanadamu hukumu, ila Bwana; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu. 7 Basi sasa hofu ya Bwana na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa Bwana, Mungu wetu, hapana uovu, wala kujali nafsi za watu, wala kupokea zawadi. 8 Tena katika Yerusalemu Yehoshafati akasimamisha wa Walawi na makuhani, na wakuu wa mbari za mababa wa Israeli wawe kwa hukumu ya Bwana, na kwa mateto. Nao wakarudi Yerusalemu. 9 Akawaagiza, akasema, Ndivyo mtakavyotenda kwa hofu ya Bwana, kwa uaminifu, na kwa moyo kamili. 10 Na kila mara watakapowajia na teto ndugu zenu wakaao mijini mwao, kati ya damu na damu, kati ya torati na amri, sheria na hukumu, mtawaonya, wasiingie hatiani mbele za Bwana, mkajiliwa na ghadhabu ninyi na ndugu zenu; fanyeni haya wala hamtakuwa na hatia. 11 Tena angalieni, Amaria, kuhani mkuu, yu juu yenu kwa maneno yote ya Bwana; naye Zebadia, mwana wa Ishmaeli, jemadari wa nyumba ya Yuda, kwa maneno yote ya mfalme; Walawi nao watakuwa wasimamizi mbele yenu. Jitieni nguvu, mtende, naye Bwana awe pamoja nao walio wema

2 Mambo ya Nyakati 20

1 Ikawa baadaye, wana wa Moabu, na wana wa Amoni, na pamoja nao baadhi ya Wameuni, wakaja juu ya Yehoshafati vitani. 2 Wakaja watu waliomwambia Yehoshafati, wakisema, Wanakuja jamii kubwa juu yako watokao Shamu toka ng'ambo ya bahari; na tazama, wako katika Hasason-tamari (ndio En-gedi). 3 Yehoshafati akaogopa, akauelekeza uso wake amtafute Bwana; akatangaza mbiu ya watu kufunga katika Yuda yote. 4 Yuda wakakusanyika pamoja ili wamtafute Bwana; hata kutoka miji yote ya Yuda wakaja kumtafuta Bwana. 5 Yehoshafati akasimama kati ya kusanyiko la Yuda na Yerusalemu, nyumbani mwa Bwana, mbele ya ua mpya; 6 akasema, Ee Bwana, Mungu wa baba zetu, si wewe uliye Mungu mbinguni? Tena si wewe utawalaye falme zote za mataifa? Na mkononi mwako mna uweza na nguvu, asiweze mtu ye yote kusimama kinyume chako. 7 Si wewe, Ee Mungu wetu, uliyewafukuza wenyeji wa nchi hii mbele ya watu wako Israeli, ukawapa wazao wa Ibrahimu rafiki yako hata milele? 8 Nao walikaa humo, wamekujengea patakatifu pa jina lako humo, wakisema, 9 Yakitujia mabaya, upanga, hukumu, au tauni, au njaa, tutasimama mbele ya nyumba hii, na mbele zako, (maana jina lako limo katika nyumba hii), na kukulilia katika shida yetu, nawe utasikia na kuokoa. 10 Na sasa, tazama, wana wa Amoni, na Moabu, na wa mlima Seiri, ambao hukuwaacha Israeli waingie katika nchi yao, walipotoka nchi ya Misri; lakini wakawageukia mbali, wasiwaharibu; 11 tazama, jinsi wanavyotulipa, wakija kututupa toka milki yako, uliyoturithisha. 12 Ee Mungu wetu, je! Hutawahukumu? Maana sisi hatuna uwezo juu ya jamii kubwa hii, wanaotujia juu yetu; wala hatujui tufanyeje; lakini macho yetu yatazama kwako. 13 Wakasimama Yuda wote mbele za Bwana, pamoja na wadogo wao, na wake zao, na watoto wao. 14 Ndipo Yahazieli mwana wa Zekaria, mwana wa Benaya, mwana wa Yeieli, mwana wa Matania, Mlawi, wa wana wa Asafu, akajiliwa na roho ya Bwana, katikati ya kusanyiko; 15 akasema, Sikieni, Yuda wote, nanyi mkaao Yerusalemu, na wewe mfalme Yehoshafati; Bwana awaambia hivi, Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu. 16 Kesho shukeni juu yao; tazameni, wanakwea kwa kupandia Sisi; nanyi mtawapata penye mwisho wa bonde, mbele ya jangwa la Yerueli. 17 Hamtahitaji kupigana vita, jipangeni, simameni, mkauone wokovu wa Bwana ulio pamoja nanyi, enyi Yuda na Yerusalemu; msiogope, wala msifadhaike; kesho tokeni juu yao; kwa kuwa Bwana yu pamoja nanyi. 18 Yehoshafati akainama kichwa, kifulifuli; wakaanguka mbele za Bwana Yuda wote na wakaao Yerusalemu, wakimsujudia Bwana. 19 Na Walawi, wa wana wa Wakohathi na wa wana wa Wakorahi, wakasimama ili wamsifu Bwana, Mungu wa Israeli, kwa sauti kuu sana. 20 Wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda nje katika jangwa la Tekoa; nao walipokuwa wakitoka, Yehoshafati akasimama, akasema, Nisikieni, enyi Yuda nanyi wenyeji wa Yerusalemu; mwaminini Bwana, Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa. 21 Naye alipokwisha kufanya shauri na watu, akawaweka wale watakaomwimbia Bwana, na kumsifu katika uzuri wa utakatifu, wakitoka mbele ya jeshi, na kusema, Mshukuruni Bwana; kwa maana fadhili zake ni za milele. 22 Nao walipoanza kuimba na kusifu, Bwana akaweka waviziao juu ya wana wa Amoni, na Moabu, na wa mlima Seiri, waliokuja juu ya Yuda; nao wakapigwa. 23 Kwani wana wa Amoni na wa Moabu waliwaondokea wenyeji wa mlima Seiri kuwaulia mbali na kuwaharibu; nao walipokwisha kuwakomesha hao wakaao Seiri, wakajitia kuharibu kila mtu mwenziwe. 24 Hata Yuda walipofika mnara wa kulindia wa jangwani, wakalitazama hilo jeshi; nao, angalia, walikuwa maiti walioanguka nchi, wala hapana aliyeokoka. 25 Nao Yehoshafati na watu wake walipokuja kuchukua nyara zao, wakaona kati yao wingi wa mali, na mavazi, na johari za thamani, walivyojivulia, zaidi kuliko wawezavyo kuchukua; wakawa siku tatu katika kuteka nyara, maana zilikuwa nyingi sana. 26 Hata siku ya nne wakakusanyika katika bonde la Baraka; maana ndipo walipombarikia Bwana; kwa hiyo jina lake mahali pale pakaitwa Bonde la Baraka hata leo. 27 Kisha wakarudi, kila mtu wa Yuda na Yerusalemu, na Yehoshafati mbele yao, ili kuurudia Yerusalemu kwa furaha; kwa kuwa Bwana amewafurahisha juu ya adui zao. 28 Wakafika Yerusalemu wenye vinanda vinubi na mapanda kwenda nyumbani kwa Bwana. 29 Ikawa hofu ya Mungu juu ya falme zote za nchi, waliposikia ya kuwa Bwana amepigana juu ya adui za Israeli. 30 Basi ukatulia ufalme wake Yehoshafati; kwa sababu Mungu wake alimstarehesha pande zote. 31 Yehoshafati akatawala juu ya Yuda; alikuwa na umri wa miaka thelathini na mitano alipoanza kutawala, akatawala miaka ishirini na mitano huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Azuba binti Shilhi. 32 Akaiendea njia ya Asa babaye, wala hakuiacha, akifanya yaliyo mema machoni pa Bwana. 33 Lakini mahali pa juu hapakuondolewa; wala mioyo ya watu bado haijakazwa kwa Mungu wa baba zao. 34 Na mambo yote ya Yehoshafati yaliyosalia, ya kwanza na ya mwisho, angalia, yameandikwa katika tarehe ya Yehu mwana wa Hanani, iliyotiwa katika kitabu cha wafalme wa Israeli. 35 Baada ya hayo Yehoshafati mfalme wa Yuda akapatana na Ahazia mfalme wa Israeli; naye huyo ndiye aliyefanya mabaya mno; 36 akapatana naye kufanya merikebu za kuendea Tarshishi; wakazifanya merikebu zile huko Esion-geberi. 37 Ndipo Eliezeri mwana wa Dodavahu wa Maresha akatoa unabii juu ya Yehoshafati, akasema, Kwa sababu umepatana na Ahazia, Bwana amezivunja-vunja kazi zako. Zikavunjika merikebu, zisiweze kufika Tarshishi.

2 Mambo ya Nyakati 21

1 Yehoshafati akalala na babaze, akazikwa pamoja na babaze katika mji wa Daudi; akatawala Yehoramu mwanawe mahali pake. 2 Naye alikuwa na ndugu, wana wa Yehoshafati, Azaria, na Yehieli, na Zekaria, na Azaria, na Mikaeli, na Shefatia; hao wote walikuwa wana wa Yehoshafati mfalme wa Israeli. 3 Baba yao akawapa zawadi kubwa, za fedha, na za dhahabu, na za tunu, pamoja na miji yenye maboma katika Yuda; lakini ufalme akampa Yehoramu, kwa sababu alikuwa mzaliwa wa kwanza. 4 Basi Yehoramu alipoinuliwa juu ya ufalme wa babaye, na kujitia nguvu, akawaua nduguze wote kwa upanga, na baadhi ya wakuu wa Israeli pia. 5 Yehoramu alikuwa na umri wa miaka thelathini na miwili alipoanza kutawala, akatawala miaka minane huko Yerusalemu. 6 Akaiendea njia ya wafalme wa Israeli, kama walivyofanya nyumba ya Ahabu; kwa kuwa alikuwa amemwoa binti Ahabu; akafanya maovu machoni pa Bwana. 7 Walakini Bwana hakupenda kuiharibu nyumba ya Daudi, kwa sababu ya agano alilolifanya na Daudi, na kama alivyomwahidi kuwa atampa taa, yeye na wazao wake siku zote. 8 Zamani zake Edomu wakaasi chini ya mkono wa Yuda, wakajifanyia mfalme. 9 Ndipo akavuka Yehoramu na maakida wake, na magari yake yote pamoja naye; akaondoka usiku, akawapiga Waedomi waliomzunguka yeye na hao maakida wa magari. 10 Hivyo Edomu wakaasi chini ya mkono wa Yuda, hata leo; wakaasi na Libna zamani zizo hizo chini ya mkono wake: kwa sababu alikuwa amemwacha Bwana, Mungu wa baba zake. 11 Tena ndiye aliyefanya mahali pa juu milimani pa Yuda, na kuwaendesha katika uasherati wenyeji wa Yerusalemu, na kuwakosesha Yuda. 12 Likamjia andiko kutoka kwa Eliya nabii, kusema, Bwana, Mungu wa Daudi baba yako, asema hivi, Kwa sababu hukuziendea njia za Yehoshafati baba yako, wala njia za Asa mfalme wa Yuda; 13 lakini umeiendea njia ya wafalme wa Israeli, ukawaendesha katika uasherati Yuda na wenyeji wa Yerusalemu, kama walivyofanya nyumba ya Ahabu; tena umewaua ndugu zako wa nyumba ya baba yako, waliokuwa wema kuliko wewe; 14 tazama, Bwana atawapiga pigo kubwa watu wako, na watoto wako, na wake zako, na mali yako yote; 15 nawe utakuwa na ugonjwa mkuu kwa maradhi ya matumbo, yatakapotokea matumbo yako kwa sababu ya ugonjwa huo siku kwa siku. 16 Bwana akawaamsha roho Wafilisti, na Waarabu waliowaelekea Wakushi juu ya Yehoramu, 17 nao wakakwea juu ya nchi ya Yuda, wakaipenya, wakaichukua mali yote iliyoonekama nyumbani mwa mfalme, na wanawe pia, na wakeze; asisaziwe mwana hata mmoja, ila Ahazia, aliyekuwa mdogo miongoni mwa wanawe. 18 Na baada ya hayo yote Bwana akampiga matumbo kwa ugonjwa usioponyeka. 19 Ikawa baada ya siku, ikiisha miaka miwili, matumbo yake yakatokea kwa sababu ya ugonjwa wake, akafa akiugua vibaya. Wala watu wake hawakumfukizia mafukizo kama ya baba zake. 20 Alikuwa na umri wa miaka thelathini na miwili alipoanza kutawala, akatawala huko Yerusalemu miaka minane; akafariki bila kutamaniwa; wakamzika mjini mwa Daudi, ila si katika makaburi ya wafalme.

2 Mambo ya Nyakati 22

1 Nao wenyeji wa Yerusalemu walimfanya Ahazia mwanawe mdogo awe mfalme mahali pake; maana wakubwa wote wamekwisha kuuawa na kikosi cha watu waliokuja matuoni pamoja na Waarabu. Hivyo akatawala Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda. 2 Ahazia alikuwa na umri wa miaka arobaini na miwili alipoanza kutawala; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Athalia binti Omri. 3 Yeye naye akaziendea njia za nyumba ya Ahabu; kwa kuwa mamaye alikuwa mshauri wake katika kufanya maovu. 4 Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana kama nyumba ya Ahabu; kwa kuwa hao walikuwa washauri wake, alipokwisha kufa babaye, hata aangamie. 5 Naye akaenda kwa mashauri yao, akafuatana na Yoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli ili kupigana na Hazaeli mfalme wa Shamu huko Ramoth-Gileadi;nao Washami wakamjeruhi Yoramu. 6 Akarudi Yezreeli ili aponye jeraha walizomjeruhi huko Rama, alipopigana na Hazaeli mfalme wa Shamu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda ,akashuka amtazame Yoramu mwana wa Ahabu,katika Yezreeli,kwa sababu alikuwa hawezi. 7 Basi kuangamia kwake Ahazia kulitokana na Mungu, kwa vile alivyomwendea Yoramu; kwa kuwa alipofika, akatoka pamoja na Yoramu juu ya Yehu mwana wa Nimshi, ambaye Bwana alimtia mafuta ili awakatilie mbali nyumba ya Ahabu. 8 Ikawa, Yehu alipokuwa akiwafanyia hukumu nyumba ya Ahabu, aliwakuta wakuu wa Yuda, na wana wa nduguze Ahazia, wakimtumikia Ahazia, akawaua. 9 Akamtafuta Ahazia, wakamkamata, (naye alikuwa amejificha Samaria,) wakamleta kwa Yehu, wakamwua; wakamzika, kwa maana wakasema, Huyu ni mwana wa Yehoshafati, huyo aliyemtafuta Bwana kwa moyo wake wote. Wala nyumba ya Ahazia hawakuwa na uwezo wa kuushika ufalme. 10 Basi Athalia, mama wa Ahazia, alipoona ya kuwa mwanawe amekufa, akainuka, akawaangamiza wazao wote wa kifalme wa nyumba ya Yuda. 11 Ila Yehosheba, binti mfalme, akamtwaa Yoashi, mwana wa Ahazia, akamwiba miongoni mwa wana wa mfalme waliouawa, akamweka yeye na yaya wake katika chumba cha kulala. Basi Yehosheba, binti mfalme Yehoramu, mkewe Yehoyada kuhani, (naye alikuwa umbu lake Ahazia,) akaficha usoni pa Athalia, asimwue. 12 Akawako pamoja nao, amefichwa nyumbani mwa Mungu, miaka sita. Na Athalia akaitawala nchi.

2 Mambo ya Nyakati 23

1 Hata mwaka wa saba Yehoyada akajitia nguvu, akawatwaa maakida wa mamia, Azaria mwana wa Yerohamu, na Ishmaeli mwana wa Yehohanani, na Azaria mwana wa Obedi, na Maaseya mwana wa Adaya, na Elishafati mwana wa Zikri, akapatana nao. 2 Wakazunguka katikati ya Yuda, wakawakusanya Walawi kutoka katika miji yote ya Yuda, na wakuu wa nyumba za mababa wa Israeli, wakaja Yerusalemu. 3 Na kusanyiko lote wakafanya agano na mfalme nyumbani mwa Mungu. Akawaambia, Angalieni, mwana wa mfalme atatawala, kama Bwana alivyonena juu ya wana wa Daudi. 4 Hili ndilo neno mtakalolifanya; theluthi yenu, ninyi mwingiao siku ya sabato, wa makuhani, na wa Walawi, mtalinda milangoni; 5 na theluthi nyumbani pa mfalme; na theluthi mlangoni pa msingi; na watu wote watakuwapo nyuani mwa nyumba ya Bwana. 6 Wala asiingie mtu nyumbani mwa Bwana, ila makuhani, na hao watumikao wa Walawi; hao wataingia, kwa kuwa hao ni watakatifu; ila watu wote watalinda malinzi ya Bwana. 7 Nao Walawi watamzunguka mfalme pande zote, kila mtu mwenye silaha zake mkononi; naye awaye yote aingiaye nyumbani na auawe; nanyi mfuatane na mfalme, aingiapo na atokapo. 8 Basi Walawi na Yuda wote wakafanya sawasawa na yote aliyowaamuru Yehoyada kuhani; wakawatwaa kila mtu watu wake, hao watakaoingia siku ya sabato, na wale watakaotoka siku ya sabato; kwa maana Yehoyada kuhani hakuzifumua zamu. 9 Naye Yehoyada kuhani akawapa maakida wa mamia mikuki, na ngao, na vigao, vilivyokuwa vya mfalme Daudi, vilivyokuwamo nyumbani mwa Mungu. 10 Akawasimamisha watu wote, kila mtu mwenye silaha yake mkononi, toka pembe ya kuume ya nyumba mpaka pembe ya kushoto, upande wa madhabahu na nyumba, kumzunguka mfalme pande zote. 11 Ndipo wakamleta nje mwana wa mfalme, wakamvika taji, na kumpa ule ushuhuda, wakamtawaza awe mfalme; Yehoyada na wanawe wakamtia mafuta, wakasema, Mfalme na aishi. 12 Na Athalia alipoisikia sauti ya watu, na ya walinzi, na ya hao waliomsifu mfalme, akaingia kwa watu nyumbani mwa Bwana; 13 akatazama, na angalia, mfalme amesimama karibu na nguzo yake mlangoni, nao maakida na wenye mapanda karibu na mfalme; wakafurahi watu wote wa nchi, wakapiga mapanda; waimbaji pia wakipiga vinanda, wakaongoza nyimbo za kusifu. Ndipo Athalia akararua mavazi yake, akasema, Fitina! Fitina! 14 Yehoyada kuhani akawaleta nje maakida wa mamia, waliowekwa juu ya jeshi, akawaambia, Mtoeni nje kati ya safu; naye ye yote amfuataye, na auawe kwa upanga; kwani kuhani amesema, Msimwue katika nyumba ya Bwana. 15 Basi wakampisha njia; akaenda kwa kuingia pa mlango wa farasi nyumbani mwa mfalme; nao wakamwua huko. 16 Kisha, Yehoyada akafanya agano, yeye na watu wote, na mfalme, kwamba watakuwa watu wa Bwana. 17 Na watu wote wakaiendea nyumba ya Baali, wakaibomoa; wakavunja-vunja madhabahu zake na sanamu zake, wakamwua Matani kuhani wa Baali mbele ya madhabahu. 18 Yehoyada akauamuru usimamizi wa nyumba ya Bwana chini ya mkono wa makuhani Walawi, aliowagawa Daudi nyumbani mwa Bwana, ili wazisongeze sadaka za kuteketezwa za Bwana, kama ilivyoandikwa katika torati ya Musa, kwa kufurahi na kuimba, kama alivyoamuru Daudi. 19 Akawasimamisha walinzi malangoni pa nyumba ya Bwana, asiingie aliye mchafu kwa vyo vyote. 20 Akawatwaa maakida wa mamia, na watu wakubwa, na hao watawalao watu, na watu wote wa nchi, akamtelemsha mfalme kutoka nyumba ya Bwana; wakalipitia lango la juu waende nyumbani kwa mfalme, wakamketisha mfalme katika kiti cha ufalme. 21 Basi wakafurahi watu wote wa nchi, na mji ukatulia; naye Athalia wakamwua kwa upanga.

2 Mambo ya Nyakati 24

1 Yoashi alikuwa na umri wa miaka saba alipoanza kutawala; akatawala miaka arobaini huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Sibia wa Beer-sheba. 2 Yoashi akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana siku zote za Yehoyada kuhani. 3 Yehoyada akamwoza wake wawili, naye akazaa wana na binti. 4 Ikawa baada ya haya, Yoashi alikuwa na nia ya kuitengeneza nyumba ya Mungu. 5 Akawakusanya makuhani na Walawi, akawaambia, Nendeni mijini mwa Yuda, mkakusanye katika Israeli wote fedha, ili kuitengeneza nyumba ya Mungu wenu mwaka kwa mwaka, mkafanye bidii kuliharakisha neno hili. Walakini Walawi hawakuliharakisha. 6 Mfalme akamwita Yehoyada mkuu wao, akamwambia, Mbona hukuwataka Walawi waitoze Yuda na Yerusalemu kodi ya Musa mtumishi wa Bwana, na ya kusanyiko la Israeli, kwa ajili ya hema ya ushuhuda? 7 Kwa kuwa wana wa Athalia, yule mwanamke mwovu, walikuwa wameibomoa nyumba ya Mungu; na vitakatifu vyote vya nyumba ya Bwana wamewapatia mabaali. 8 Basi mfalme akaamuru, nao wakafanyiza kasha, wakaliweka nje langoni pa nyumba ya Bwana. 9 Wakapiga mbiu katika Yuda na Yerusalemu, kumletea Bwana kodi aliyoiweka Musa mtumishi wa Mungu, juu ya Israeli jangwani. 10 Wakafurahi maakida wote na watu wote, wakaleta na kutia ndani ya kasha, hata wakaisha. 11 Ikawa wakati walipoletewa kasha wasimamizi wa mfalme kwa mkono wa Walawi, nao wakaona ya kwamba kuna fedha nyingi, huja karani wa mfalme, na msimamizi wake kuhani mkuu, wakatoa yaliyomo kashani, kisha hulichukua kasha, na kulirudisha mahali pake. Ndivyo walivyofanya siku kwa siku, wakakusanya fedha tele. 12 Na mfalme na Yehoyada waliwapa hao waliofanya kazi ya utumishi wa nyumba ya Bwana; nao wakawaajiri waashi na maseremala ili kuitengeza nyumba ya Bwana, na hao pia wafuao chuma na shaba ili kuitengeza nyumba ya Bwana. 13 Hivyo mafundi wakafanya kazi yao, nao wakaimaliza, wakaisimamisha nyumba ya Mungu kama ilivyopasa, wakaifanya imara. 14 Nao walipokwisha, wakaleta mbele ya mfalme na Yehoyada fedha iliyobaki, vikafanyizwa kwayo vyombo vya nyumba ya Bwana, vyombo vya utumishi, navyo vya kutolea, na miiko, na vyombo vya dhahabu na fedha. Wakatoa sadaka za kuteketezwa katika nyumba ya Bwana, daima, siku zote za Yehoyada. 15 Lakini Yehoyada akawa mzee, mwenye umri mwingi, akafa; alipokufa alikuwa na umri wa miaka mia na thelathini. 16 Wakamzika katika mji wa Daudi kati ya wafalme, kwa sababu ametenda mema katika Israeli, na kwa Mungu, na katika nyumba yake. 17 Hata baada ya kufa kwake Yehoyada, wakuu wa Yuda wakamwendea mfalme, wakamsujudia. Naye mfalme akawasikiliza maneno yao. 18 Wakaiacha nyumba ya Bwana, Mungu wa baba zao; wakatumikia maashera na sanamu; ghadhabu ikawajia Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hiyo hatia yao. 19 Hata hivyo akawapelekea manabii, ili kuwarudisha kwa Bwana; nao wakawashuhudia; lakini hawakukubali kuwasikiliza. 20 Na roho ya Mungu ikamjia Zekaria, mwana wa Yehoyada, kuhani; naye akasimama juu ya watu, akawaambia, Mungu asema hivi, Kwani ninyi kuzihalifu amri za Bwana, hata msiweze kufanikiwa? Kwa kuwa mmemwacha Bwana, yeye naye amewaacha ninyi. 21 Basi, wakafanya shauri juu yake, wakampiga kwa mawe kwa amri ya mfalme katika ua wa nyumba ya Bwana. 22 Basi hivyo mfalme Yoashi hakuukumbuka wema, ambao Yehoyada, baba yake, alimfanyia, bali alimwua mwanawe. Naye alipokufa, alisema, Bwana na ayaangalie haya, akayatakie kisasi. 23 Ikawa mwisho wa mwaka, wakakwea juu yake jeshi la Washami; wakafika Yuda na Yerusalemu, wakawaangamiza wakuu wa watu wote miongoni mwa watu, wakamletea mfalme wa Dameski nyara zao zote. 24 Maana wakaja jeshi la Washami watu haba; Bwana akatia mikononi mwao jeshi kubwa mno, kwa sababu wamemwacha Bwana, Mungu wa baba zao. Hivyo wakamfanyia Yoashi hukumu. 25 Hata walipoondoka kwake, (nao walimwacha ameshikwa sana na maradhi,) watumishi wake mwenyewe wakamfanyia fitina kwa ajili ya damu ya mwana wa Yehoyada kuhani, wakamwua kitandani pake, akafa; wakamzika mjini mwa Daudi, lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme. 26 Na hawa ndio waliomfanyia fitina, Zabadi mwana wa Shimeathi mwanamke Mwamoni, na Yehozabadi mwana wa Shimrithi mwanamke Mmoabi. 27 Basi kwa habari ya wanawe, na ukubwa wa mizigo aliolemewa, na majengo ya nyumba ya Mungu, tazama, hayo yameandikwa katika maelezo ya kitabu cha wafalme. Na Amazia mwanawe akatawala mahali pake.

2 Mambo ya Nyakati 25

1 Amazia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka ishirini na kenda; na jina la mamaye aliitwa Yehoadani wa Yerusalemu. 2 Akafanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, lakini si kwa moyo mkamilifu. 3 Basi ikawa, alipopata nguvu katika ufalme wake, akawaua watumishi wale waliomwua mfalme babaye. 4 Lakini watoto wao hakuwaua, ila alifanya sawasawa na hayo yaliyoandikwa katika torati, katika kitabu cha Musa, kama Bwana alivyoamuru, akisema, Mababa wasife kwa makosa ya wana, wala wana wasife kwa makosa ya mababa; lakini kila mtu atakufa kwa dhambi yake mwenyewe. 5 Tena Amazia akawakusanya Yuda, akawaweka sawasawa na nyumba za baba zao chini ya maakida wa maelfu, na maakida wa mamia, naam, Yuda pia, na Benyamini; tangu wenye miaka ishirini na zaidi akawahesabu, akawaona kuwa watu wateule mia tatu elfu, wawezao kwenda vitani, waliozoea mkuki na ngao. 6 Akaajiri pia watu mashujaa mia elfu wa Israeli kwa talanta mia za fedha. 7 Lakini mtu wa Mungu akamjia, akasema, Ee mfalme, usiwaache jeshi la Israeli waende nawe; kwa kuwa Bwana hayupo pamoja na Israeli, yaani, wana wote wa Efraimu. 8 Lakini ukitaka kwenda, haya, jitie nguvu upigane; Mungu atakuangusha mbele ya adui; maana Mungu anazo nguvu za kusaidia, na kuangusha. 9 Amazia akamwambia mtu wa Mungu, Lakini tuzifanyieje zile talanta mia nilizowapa jeshi la Israeli? Mtu wa Mungu akajibu, Bwana aweza kukupa zaidi sana kuliko hizo. 10 Ndipo Amazia akawafarakisha jeshi lililomjia kutoka Efraimu, ili warudi kwao; kwa hiyo ikawaka sana hasira yao juu ya Yuda, nao wakarudi kwao wenye hasira kali. 11 Amazia akapiga moyo konde, akawaongoza watu wake, akaenda mpaka Bonde la Chumvi, akawapiga katika wana wa Seiri watu elfu kumi. 12 Na elfu kumi wengine, ambao wana wa Yuda waliwachukua wali hai, wakawaleta juu ya jabali, wakawaangusha toka juu ya jabali, hata wakavunjika-vunjika wote. 13 Lakini wale watu wa jeshi, aliowarudisha Amazia, wasiende naye vitani, hao wakaiteka miji ya Yuda, tangu Samaria mpaka Beth-horoni, wakawapiga watu elfu tatu, wakachukua nyara nyingi. 14 Basi ikawa, Amazia alipokwisha rudi kutoka kuwaua Waedomi, alileta miungu ya wana wa Seiri, akaisimamisha kuwa miungu yake, akajiinama mbele yao, akaifukizia uvumba. 15 Kwa hiyo hasira ya Bwana ikawaka juu ya Amazia, akampelekea nabii, aliyemwambia, Mbona umeitafuta miungu ya watu, isiyowaokoa watu wao mkononi mwako? 16 Ikawa, aliposema naye, mfalme akamwambia, Je! Tumekutia wewe kuwa mshauri wa mfalme? Nyamaza; kwa nini upigwe? Ndipo yule nabii akaacha, akasema, Najua ya kuwa Mungu amekusudia kukuangamiza, kwa sababu umeyafanya haya, wala hukulisikiliza shauri langu. 17 Ndipo mfalme Amazia akafanya shauri, akatuma wajumbe kwa Yehoashi, mwana wa Yehoahazi mwana wa Yehu,mfalme wa Israeli,kusema,njoo,tutazamane uso kwa uso. 18 Na Yehoashi mfalme wa Israeli akatuma wajumbe kwa Amazia mfalme wa Yuda, kusema, Mbaruti uliokuwako Lebanoni ukatuma kwa mwerezi uliokuwako Lebanoni kusema, Umwoze mwanangu binti yako; kukapita hayawani aliyekuwako Lebanoni, akaukanyaga ule mbaruti. 19 Wasema, Tazama, umewapiga Edomu; na moyo wako wakutukuza ujisifu; kaa nyumbani mwako basi; mbona unataka kujitia bure katika madhara, hata uanguke, wewe na Yuda pamoja nawe? 20 Lakini Amazia hakutaka kusikia, kwa maana hayo yalitoka kwa Mungu, ili awatie mikononi mwao, kwa kuwa wameitafuta miungu ya Edomu. 21 Basi Yehoashi mfalme wa Israeli akakwea; wakatazamana uso kwa uso, yeye na Amazia mfalme wa Yuda huko Beth-shemeshi, ulio wa Yuda. 22 Yuda wakashindwa mbele ya Israeli; wakakimbia kila mtu hemani kwake. 23 Yehoashi mfalme wa Israeli akamtwaa Amazia mfalme wa Yuda, mwana wa Yoashi, mwana wa Ahazia, huko Beth-shemeshi,akamchukua mpaka Yerusalemu ,akauvunja ukuta wa Yerusalemu , toka lango la Efraimu mpaka lango la pembeni ,mikono mia nne. 24 Akaitwaa dhahabu yote, na fedha, na vyombo vyote vilivyoonekana nyumbani mwa Mungu kwa Obed-edomu, na hazina za nyumba ya mfalme, tena watu kuwa amana, akarudi Samaria. 25 Naye Amazia mwana wa Yoashi mfalme wa Yuda, akaishi baada ya kufa kwake Yehoashi mwana wa Yehoahazi, mfalme wa Israeli, miaka kumi na mitano. 26 Na mambo yote ya Amazia yaliyosalia, ya kwanza na ya mwisho, tazama, je! Hayakuandikwa katika kitabu cha wafalme wa Yuda na Israeli? 27 Basi, toka wakati alipogeuka Amazia katika kumfuata Bwana, wakamfanyia fitina katika Yerusalemu; naye akakimbia mpaka Lakishi; lakini wakatuma kumfuata mpaka Lakishi, wakamwua huko. 28 Wakamleta juu ya farasi; wakamzika pamoja na babaze katika mji wa Yuda.

2 Mambo ya Nyakati 26

1 Na watu wote wa Yuda wakamtwaa Uzia, naye alikuwa mwenye miaka kumi na sita, wakamfanya awe mfalme mahali pa Amazia babaye. 2 Huyo akajenga Elathi, akaurudisha kwa Yuda, baada ya kulala mfalme pamoja na babaze. 3 Uzia alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala; akatawala huko Yerusalemu miaka hamsini na miwili; na jina la mamaye aliitwa Yekolia wa Yerusalemu. 4 Akafanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyafanya Amazia babaye. 5 Akajitia nia amtafute Mungu katika siku za Zekaria, aliyekuwa na fahamu katika maono ya Mungu; na muda alipomtafuta Bwana, Mungu alimfanikisha. 6 Akatoka akapigana na Wafilisti, akauvunja ukuta wa Gathi, na ukuta wa Yabne, na ukuta wa Ashdodi; akajenga miji katika Ashdodi na katikati ya Wafilisti. 7 Mungu akamsaidia juu ya Wafilisti, na juu ya Waarabu waliokaa Gur-baali, na juu ya Wameuni. 8 Na Waamoni wakampa Uzia zawadi; likaenea jina lake mpaka pa kuingilia Misri; kwa kuwa akaongezeka nguvu mno. 9 Tena Uzia akaujengea Yerusalemu minara, penye lango la pembeni, na penye lango la bonde, na ugeukapo ukuta, akaitia nguvu. 10 Akajenga minara tena nyikani, akachimba mabirika mengi, maana alikuwa na ng'ombe tele; katika Shefela pia, na katika nchi tambarare; tena alikuwa na wakulima na watunza mizabibu milimani, na katika mashamba ya neema; maana yeye alipenda ukulima. 11 Zaidi ya hayo Uzia alikuwa na jeshi la watu wa kupigana, waliokwenda vitani vikosi vikosi, sawasawa na hesabu walivyohesabiwa na Yeieli mwandishi, na Maaseya msimamizi, chini ya mkono wa Hanania, mmojawapo wa maakida wa mfalme. 12 Hesabu yote ya wakuu wa nyumba za mababa, watu mashujaa, ilikuwa elfu mbili na mia sita. 13 Na chini ya mkono wao kulikuwa na jeshi la askari, mia tatu na saba elfu, na mia tano, ambao walipigana vita kwa nguvu nyingi, kumsaidia mfalme juu ya adui. 14 Uzia akawafanyizia jeshi lote ngao na mikuki, na chapeo, na deraya za madini, na nyuta, na mawe ya kupiga kwa teo. 15 Akafanya katika Yerusalemu mitambo ya vita, iliyobuniwa na watu wastadi, iwekwe juu ya minara na juu ya buruji, ili kutupa mishale na mawe makubwa. Jina lake likaenea mbali sana; kwa kuwa alisaidiwa mno ajabu, hata akapata nguvu. 16 Lakini alipokuwa na nguvu, moyo wake ulitukuka, hata akafanya maovu, akamwasi Bwana, Mungu wake; kwani aliingia hekaluni mwa Bwana, ili afukize uvumba juu ya madhabahu ya kufukizia. 17 Azaria kuhani akaingia nyuma yake, na pamoja naye makuhani themanini wa Bwana, mashujaa; 18 wakamzuia Uzia mfalme, wakamwambia, Si haki yako, Uzia, kumfukizia Bwana uvumba, ila ni haki ya makuhani wana wa Haruni, waliofanywa wakfu, ili wafukize uvumba; toka katika patakatifu; kwa kuwa umekosa; wala haitakuwa kwa heshima yako kutoka kwa Bwana, Mungu. 19 Akaghadhibika Uzia; naye alikuwa na chetezo mkononi cha kufukizia uvumba; naye hapo alipowaghadhibikia makuhani, ukamtokea ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani nyumbani mwa Bwana karibu na madhabahu ya kufukizia. 20 Azaria kuhani mkuu na makuhani wote wakamtazama, na angalia, alikuwa na ukoma pajini mwa uso, wakamtoa humo upesi; hata na yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa sababu Bwana amempiga. 21 Uzia mfalme akawa na ukoma hata siku ya kufa kwake, akakaa katika nyumba ya pekee, kwa kuwa ni mwenye ukoma; maana alitengwa na nyumba ya Bwana; na Yothamu mwanawe alikuwa juu ya nyumba ya mfalme, akiwahukumu watu wa nchi. 22 Basi mambo yote ya Uzia yaliyosalia, ya kwanza na ya mwisho, aliyaandika Isaya nabii, mwana wa Amozi. 23 Basi Uzia akalala na babaze; wakamzika pamoja na babaze katika konde la kuzikia la wafalme; kwa kuwa walisema, Huyu ni mwenye ukoma. Na Yothamu mwanawe akatawala mahali pake

2 Mambo ya Nyakati 27

1 Yothamu alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka kumi na sita; na jina la mamaye aliitwa Yerusha binti Sadoki. 2 Akafanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyafanya Uzia babaye; isipokuwa hakuingia hekaluni mwa Bwana. Lakini watu walikuwa wakali kufanya maovu. 3 Ndiye aliyelijenga lango la juu la nyumba ya Bwana, na juu ya ukuta wa Ofeli akajenga sana. 4 Tena akajenga miji katika milima ya Yuda, na mwituni akajenga ngome na minara. 5 Kisha akapigana na mfalme wa wana wa Amoni, akawashinda. Na wana wa Amoni wakampa mwaka ule ule talanta mia za fedha, na kori elfu kumi za ngano, na elfu kumi za shayiri. Hayo ndiyo waliyomtolea wana wa Amoni, mwaka wa pili pia, na mwaka wa tatu. 6 Basi Yothamu akawa na nguvu, kwa kuwa alizitengeneza njia zake mbele za Bwana, Mungu wake. 7 Na mambo yote ya Yothamu yaliyosalia, na vita vyake vyote, na njia zake, tazama, yameandikwa katika kitabu cha wafalme wa Israeli na Yuda. 8 Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka kumi na sita huko Yerusalemu. 9 Yothamu akalala na babaze, wakamzika katika mji wa Daudi; na Ahazi mwanawe akatawala mahali pake.

2 Mambo ya Nyakati 28

1 Ahazi alikuwa na umri wa miaka ishirini alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka kumi na sita; wala hakufanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, kama Daudi babaye; 2 bali akaziendea njia za wafalme wa Israeli, akawafanyizia mabaali sanamu za kusubu. 3 Tena akafukiza uvumba katika bonde la mwana wa Hinomu, akawateketeza wanawe motoni, sawasawa na machukizo ya mataifa, aliowafukuza Bwana mbele ya wana wa Israeli. 4 Akatoa dhabihu na kufukiza uvumba katika mahali pa juu, na vilimani, na chini ya kila mti wenye majani mabichi. 5 Kwa hiyo Bwana, Mungu wake, akamtia mkononi mwa mfalme wa Shamu; wakampiga, wakachukua wa watu wake wafungwa wengi sana, wakawaleta Dameski. Tena akatiwa mkononi mwa mfalme wa Israeli, aliyempiga mapigo makuu. 6 Kwa kuwa Peka mwana wa Remalia akawaua katika Yuda siku moja watu mia na ishirini elfu, mashujaa wote; kwa sababu walikuwa wamemwacha Bwana, Mungu wa baba zao. 7 Naye Zikri, mtu hodari wa Efraimu, akawaua Maaseya mwana wa mfalme, na Azrikamu mkuu wa nyumba, na Elkana, aliyekuwa wa pili wake mfalme. 8 Wana wa Israeli wakachukua wa ndugu zao wafungwa mia mbili elfu, wanawake, na wana, na binti, pia wakachukua kwao nyara nyingi, wakazileta nyara Samaria. 9 Lakini kulikuwako huko nabii wa Bwana, jina lake aliitwa Odedi; akatoka kuwalaki jeshi waliokuja Samaria, akawaambia, Angalieni, kwa kuwa Bwana, Mungu wa baba zenu, aliwakasirikia Yuda, yeye amewatia mikononi mwenu, nanyi mmewaua kwa ghadhabu iliyofikia mbinguni. 10 Na sasa mwanuia kuwatawala wana wa Yuda na Yerusalemu, wawe kwenu watumwa na wajakazi; lakini ninyi nanyi je! Hamna hatia zenu wenyewe juu ya Bwana, Mungu wenu? 11 Haya, nisikieni mimi basi, mwarudishe wafungwa, mliowachukua mateka wa ndugu zenu; kwa maana ghadhabu ya Bwana iliyo kali i juu yenu. 12 Ndipo wakaondoka juu ya hao waliotoka vitani baadhi ya wakuu wa wana wa Efraimu, Azaria, mwana wa Yohanani, na Berekia mwana wa Meshilemothi, na Yehizkia mwana wa Shalumu, na Amasa mwana wa Hadlai, 13 wakawaambia, Hamtawaleta wafungwa humo; kwa sababu mnayanuia yatakayotutia hatiani mbele za Bwana, kuongeza dhambi zetu, na hatia yetu; maana hatia yetu ni kubwa, na ghadhabu kali ipo juu ya Israeli. 14 Basi watu wenye silaha wakawaacha wafungwa na nyara mbele ya wakuu na kusanyiko lote. 15 Wakaondoka wale watu waliotajwa majina yao, wakawatwaa wafungwa, wakawavika kwa zile nyara wote wao waliokuwa uchi, wakawapa mavazi na viatu, wakawalisha, wakawanywesha, wakawatia mafuta, wakawapandisha waliokuwa dhaifu miongoni mwao juu ya punda wakawaleta Yeriko, mji wa mitende, kwa ndugu zao; kisha wakarudi Samaria. 16 Wakati ule mfalme Ahazi akatuma wajumbe kwa mfalme wa Ashuru ili amsaidie. 17 Kwa kuwa Waedomi walikuwa wamekuja tena, na kuwapiga Yuda, na kuwachukua wafungwa. 18 Wafilisti pia walikuwa wameingia miji ya Shefela, na ya Negebu ya Yuda, nao wameutwaa Beth-shemeshi, na Ayaloni, na Gederothi, na Soko pamoja na miji yake, na Timna pamoja na miji yake, na Gimzo pia na miji yake; wakakaa humo. 19 Kwa maana Bwana aliinamisha Yuda kwa ajili ya Ahazi mfalme wa Israeli; kwa kuwa yeye aliwafanyia Yuda aibu, na kumwasi Bwana mno. 20 Na Tiglath-pileseri mfalme wa Ashuru akamjia, akamfadhaisha, asimtie nguvu kwa lo lote. 21 Kwa maana Ahazi alitwaa sehemu katika nyumba ya Bwana, na katika nyumba ya mfalme, na ya wakuu, akampa mfalme wa Ashuru; asisaidiwe na jambo hilo. 22 Na wakati alipofadhaishwa, akazidi kumwasi Bwana, huyo mfalme Ahazi. 23 Kwani akaitolea dhabihu miungu ya Dameski iliyompiga, akasema, Kwa sababu miungu ya wafalme wa Shamu imewasaidia wao, mimi nitaitolea dhabihu, ili inisaidie mimi. Lakini ndiyo iliyomwangamiza yeye na Israeli wote. 24 Tena Ahazi akakusanya vyombo vyote vya nyumba ya Mungu, akavikata vipande vipande vyombo vya nyumba ya Mungu, akaifunga milango ya nyumba ya Bwana; akajifanyizia madhabahu katika kila pembe ya Yerusalemu. 25 Na katika kila mji wa Yuda akafanya mahali pa juu pa kuifukizia miungu mingine uvumba, akamkasirisha Bwana, Mungu wa babaze. 26 Basi mambo yake yote yaliyosalia, na njia zake zote, za kwanza na za mwisho, tazama, yameandikwa katika kitabu cha wafalme wa Yuda na Israeli. 27 Ahazi akalala na babaze, wakamzika mjini, yaani, Yerusalemu; maana hawakumleta makaburini mwa wafalme wa Israeli; na Hezekia mwanawe akatawala mahali pake.

2 Mambo ya Nyakati 29

1 Hezekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka ishirini na kenda; na jina la mamaye aliitwa Abiya binti Zekaria. 2 Akafanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyafanya Daudi babaye. 3 Yeye, katika mwaka wa kwanza wa kutawala kwake, katika mwezi wa kwanza, aliifungua milango ya nyumba ya Bwana, akaitengeneza. 4 Akawaingiza makuhani na Walawi, akawakusanya uwandani upande wa mashariki, 5 akawaambia, Nisikieni, enyi Walawi; jitakaseni nafsi zenu sasa, mkaitakase na nyumba ya Bwana, Mungu wa baba zenu, mkautoe uchafu katika patakatifu. 6 Kwa maana baba zetu wameasi, na kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, Mungu wetu, wamemwacha, na kugeuzia mbali nyuso zao na makao ya Bwana, na kumpa maungo. 7 Tena wameifunga milango ya ukumbi, na kuzizima taa, wala hawakufukiza uvumba, wala hawakumtolea Mungu wa Israeli sadaka za kuteketezwa katika patakatifu. 8 Kwa hiyo hasira ya Bwana imekuwa juu ya Yuda na Yerusalemu, naye amewatoa kuwa matetemeko, wawe ushangao, na mazomeo, kama mwonavyo kwa macho yenu. 9 Kwa kuwa, tazama, baba zetu wameangamia kwa upanga, na wana wetu, na binti zetu, na wake zetu wametekwa kwa ajili ya hayo. 10 Basi nia yangu ni kufanya agano na Bwana, Mungu wa Israeli, ili kwamba hasira yake kali itugeukie mbali. 11 Basi wanangu, msijipurukushe sasa, kwa kuwa Bwana amewachagua ninyi msimame mbele yake, kumhudumia, nanyi mpate kuwa watumishi wake, mkafukize uvumba. 12 Ndipo wakaondoka Walawi, Mahathi mwana wa Amasai, na Yoeli mwana wa Azaria, wa wana wa Wakohathi; na wa wana wa Merari, Kishi mwana wa Abdi, na Azaria mwana wa Yehaleleli; na wa Wagershoni, Yoa mwana wa Zima na Edeni mwana wa Yoa; 13 na wa wana wa Elisafani, Shimri na Yeueli; na wa wana wa Asafu, Zekaria na Matania; 14 na wa wana wa Hemani, Yehueli na Shimei; na wa wana wa Yeduthuni, Shemaya na Uzieli. 15 Wakawakusanya ndugu zao, wakajitakasa, wakaingia, kama alivyoamuru mfalme kwa maneno ya Bwana, ili waisafishe nyumba ya Bwana. 16 Nao makuhani wakaingia nyumbani mwa Bwana, katika mahali pa ndani, ili waisafishe, wakatoa uchafu wote waliouona hekaluni mwa Bwana, wakautupa nje uani mwa nyumba ya Bwana. Walawi wakautwaa, ili wauchukue nje mpaka kijito cha Kidroni. 17 Basi wakaanza kutakasa siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, hata siku ya nane ya mwezi wakafika katika ukumbi wa Bwana; wakaitakasa nyumba ya Bwana katika muda wa siku nane; wakamaliza siku ya kumi na sita ya mwezi wa kwanza. 18 Wakaingia ndani kwa Hezekia mfalme, wakasema, Tumeisafisha nyumba yote ya Bwana, na madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, pamoja na vyombo vyake vyote, na meza ya mikate ya wonyesho, pamoja na vyombo vyake vyote. 19 Tena vyombo vyote alivyovitupa mfalme Ahazi alipotawala, hapo alipoasi, tumevitengeza na kuvitakasa; navyo, tazama, vipo mbele ya madhabahu ya Bwana. 20 Ndipo Hezekia mfalme akaamka mapema, akakusanya wakuu wa mji, akapanda nyumbani kwa Bwana. 21 Wakaleta ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba, na wana-kondoo saba, na mabeberu saba, kuwa sadaka ya dhambi kwa ajili ya ufalme, na kwa ajili ya patakatifu, na kwa ajili ya Yuda. Akaamuru makuhani, wana wa Haruni, wawatoe madhabahuni pa Bwana. 22 Basi wakawachinja ng'ombe, na makuhani wakaipokea damu, wakainyunyiza madhabahuni; wakawachinja kondoo waume, na kuinyunyiza damu madhabahuni; wakawachinja na wana-kondoo, na kuinyunyiza damu madhabahuni. 23 Wakawaleta karibu mabeberu wa sadaka ya dhambi mbele ya mfalme na kusanyiko; wakawawekea mikono yao; 24 na makuhani wakawachinja, wakaitoa damu yao kuwa sadaka ya dhambi madhabahuni, ili kuwafanyia Israeli wote upatanisho; maana mfalme aliamuru Israeli wote wafanyiwe sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya dhambi. 25 Akawasimamisha Walawi nyumbani mwa Bwana wenye matoazi, wenye vinanda, na wenye vinubi, kama alivyoamuru Daudi, na Gadi mwonaji wa mfalme, na Nathani nabii; kwani Bwana aliamuru hivi kwa manabii wake. 26 Wakasimama Walawi wenye vinanda vya Daudi, na makuhani wenye mapanda. 27 Hezekia akaamuru kutoa sadaka ya kuteketezwa madhabahuni. Na wakati ilipoanza sadaka hiyo ya kuteketezwa, ukaanza na huo wimbo wa Bwana, na mapanda, pamoja na vinanda vya Daudi mfalme wa Israeli. 28 Na kusanyiko lote wakaabudu, waimbaji wakaimba, wenye mapanda wakapiga; haya yote yakaendelea hata ilipomalizika sadaka ya kuteketezwa. 29 Hata walipokwisha kutoa sadaka, mfalme, na hao wote waliokuwapo naye, wakasujudia, wakaabudu. 30 Tena Hezekia mfalme na wakuu wakawaamuru Walawi, wamwimbie Bwana sifa kwa maneno ya Daudi, na ya Asafu mwonaji. Wakaimba sifa kwa furaha, wakainama vichwa, wakaabudu. 31 Ndipo Hezekia akajibu, akasema, Sasa mmejifanya wakfu kwa Bwana, karibuni mkalete dhabihu na matoleo ya shukrani nyumbani mwa Bwana. Basi kusanyiko wakaleta dhabihu na matoleo ya shukrani; na wote wenye moyo wa ukarimu, wakaleta sadaka za kuteketezwa. 32 Na hesabu ya sadaka hizo za kuteketezwa walizozileta kusanyiko ikawa ng'ombe waume sabini, kondoo waume mia, na wana-kondoo mia mbili; hao wote walikuwa ni sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana. 33 Na vitu vitakatifu vilikuwa ng'ombe mia sita, na kondoo elfu tatu. 34 Lakini makuhani walikuwa wachache, wasiweze kuchuna sadaka zote za kuteketezwa; basi ndugu zao Walawi wakawasaidia, hata ilipokwisha kazi, na hata makuhani walipojitakasa; kwa kuwa Walawi walikuwa wenye mioyo ya adili kwa kujitakasa kuliko makuhani. 35 Na tena sadaka za kuteketezwa nazo zilikuwa nyingi, pamoja na mafuta ya sadaka za amani, na sadaka za kinywaji kwa kila sadaka ya kuteketezwa. Hivyo ikatengezeka huduma ya nyumba ya Bwana. 36 Akafurahi Hezekia, na watu wote, kwa sababu ya hayo Mungu aliyowatengenezea watu; maana jambo hilo likawa kwa ghafula.

2 Mambo ya Nyakati 30

1 Hezekia akatuma wajumbe kwa Israeli wote na Yuda pia; akawaandikia nyaraka Efraimu na Manase, waje nyumbani kwa Bwana Yerusalemu, ili wamfanyie pasaka Bwana, Mungu wa Israeli. 2 Kwa maana mfalme na wakuu wake, na kusanyiko lote katika Yerusalemu walifanya shauri kufanya pasaka mwezi wa pili. 3 Kwa sababu hawakuweza kuifanya wakati ule, kwa kuwa makuhani walikuwa hawajajitakasa wa kutosha, wala watu hawajakusanyika huko Yerusalemu. 4 Likawa neno jema machoni pa mfalme, na kusanyiko lote. 5 Basi wakafanya amri kupiga mbiu kati ya Israeli yote, toka Beer-sheba mpaka Dani, ya kwamba watu waje wamfanyie pasaka Bwana, Mungu wa Israeli, huko Yerusalemu; maana tangu siku nyingi hawakuifanya kama vile ilivyoandikwa. 6 Wakaenda matarishi wenye nyaraka za mfalme na wakuu wake, kati ya Israeli yote na Yuda, na kwa amri ya mfalme, kusema, Enyi wana wa Israeli, mrudieni Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na Isaka, na Israeli, apate kuwarudia waliosalia wenu waliookoka mikononi mwa wafalme wa Ashuru. 7 Wala msiwe kama baba zenu, na kama ndugu zenu, waliomwasi Bwana, Mungu wa baba zao, hata akawatoa kuwa ushangao, kama mwonavyo. 8 Msiwe sasa wenye shingo ngumu kama baba zenu; lakini mjitoe kwa Bwana, mkaingie katika patakatifu pake, alipopatakasa milele, mkamtumikie Bwana, Mungu wenu, hasira yake kali iwageukie mbali. 9 Kwa kuwa mkimrudia Bwana, ndugu zenu na watoto wenu watahurumiwa machoni pa hao waliowachukua mateka, nao watairudia nchi hii; kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye mwenye neema, na mwenye rehema, wala hatawageuzia mbali uso wake, mkimrudia. 10 Basi matarishi wakapita mji kwa mji kati ya nchi ya Efraimu na Manase, hata kufika Zabuloni; lakini waliwacheka-cheka, na kuwadhihaki. 11 Ila watu wengine wa Asheri, na wa Manase, na wa Zabuloni walijinyenyekeza, wakaja Yerusalemu. 12 Tena katika Yuda mkono wa Mungu ulikuwa ukiwapa moyo mmoja, waitimize amri ya mfalme na wakuu kwa neno la Bwana. 13 Basi wakakusanyika Yerusalemu watu wengi ili kuifanya sikukuu ya mikate isiyochachwa katika mwezi wa pili, kusanyiko kuu sana. 14 Wakainuka, wakaziondoa madhabahu zilizokuwamo Yerusalemu, nazo madhabahu za kufukizia wakaziondoa, wakazitupa katika kijito Kidroni. 15 Kisha wakaichinja pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi wa pili, nao makuhani na Walawi wakatahayarika, wakajitakasa, wakaleta sadaka za kuteketezwa nyumbani mwa Bwana. 16 Wakasimama mahali pao kwa taratibu yao, sawasawa na torati ya Musa, mtu wa Mungu; nao makuhani wakainyunyiza damu, waliyoipokea mikononi mwa Walawi. 17 Kwa maana kulikuwa na wengi katika kusanyiko ambao hawajajitakasa; kwa hiyo Walawi wakamchinjia pasaka, kila mtu asiyekuwa safi, ili kuwatakasa kwa Bwana. 18 Kwani wingi wa watu, naam, wengi wa Efraimu, na wa Manase, na wa Isakari, na wa Zabuloni, hawakujisafisha, lakini wakala pasaka, ila si kama ilivyoandikwa. Naye Hezekia alikuwa amewaombea, akisema, Bwana mwema na amsamehe kila mtu, 19 aukazaye moyo wake kumtafuta Mungu, Bwana, Mungu wa babaze, hata ikiwa si kwa utakaso wa patakatifu. 20 Bwana akamsikia Hezekia, akawaponya watu. 21 Nao wana wa Israeli waliohudhuria Yerusalemu wakafanya sikukuu ya mikate isiyochachwa siku saba kwa furaha kubwa; Walawi na makuhani wakamsifu Bwana siku kwa siku, wakimwimbia Bwana kwa vinanda vyenye sauti kuu. 22 Hezekia akawafurahisha mioyo Walawi wote waliokuwa wastadi wa kumtumikia Bwana. Basi muda wa siku saba wakala sikukuu, wakitoa dhabihu za sadaka za amani, na kumtolea shukrani Bwana, Mungu wa baba zao. 23 Na kusanyiko lote wakafanya shauri kufanya sikukuu siku saba nyingine; wakafanya sikukuu siku saba nyingine kwa furaha. 24 Maana Hezekia, mfalme wa Yuda, aliwatolea kusanyiko matoleo ya ng'ombe elfu, na kondoo elfu saba; na wakuu wakawatolea kusanyiko ng'ombe elfu, na kondoo elfu kumi; tena wakajitakasa makuhani wengi sana. 25 Na kusanyiko lote la Yuda, pamoja na makuhani na Walawi, na kusanyiko lote waliotoka Israeli, na wageni waliotoka katika nchi ya Israeli, nao waliokaa Yuda, wakafurahi. 26 Ikawa furaha kuu katika Yerusalemu; kwa sababu tangu siku za Sulemani mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli, hayajakuwako mambo kama hayo huko Yerusalemu. 27 Ndipo wakasimama makuhani Walawi, wakawabariki watu; ikasikiwa sauti yao, sala yao ikafika hata makao yake matakatifu, yaani, mbinguni.

2 Mambo ya Nyakati 31

1 Basi hayo yote yalipokwisha, wakatoka Israeli wote waliokuwako waende miji ya Yuda, wakazivunja-vunja nguzo, wakayakata-kata maashera, wakabomoa mahali pa juu na madhabahu katika Yuda yote na Benyamini, katika Efraimu pia na Manase, hata walipokwisha kuviharibu vyote. Ndipo wana wa Israeli wote wakarudi, kila mtu kwa milki yake, mijini kwao. 2 Hezekia akaziweka zamu za makuhani na Walawi kwa zamu zao, kila mtu kwa kadiri ya huduma yake, makuhani na Walawi pia, kwa sadaka za kuteketezwa na kwa sadaka za amani, kutumika, na kushukuru, na kusifu, malangoni mwa matuo ya Bwana. 3 Tena akaweka sehemu ya mfalme ya mali zake kwa sadaka za kuteketezwa, yaani, sadaka za kuteketezwa za asubuhi na jioni, na sadaka za kuteketezwa za sabato, na za mwezi mpya, na sikukuu, kama ilivyoandikwa katika torati ya Bwana. 4 Tena akawaamuru watu waliokaa Yerusalemu, watoe sehemu ya makuhani na Walawi, ili hao wajibidiishe katika torati ya Bwana. 5 Mara ilipotangaa amri, wana wa Israeli wakatoa kwa wingi malimbuko ya nafaka, na divai, na mafuta, na asali, na mazao yote ya mashamba; na zaka za vitu vyote wakazileta nyingi. 6 Nao wana wa Israeli na Yuda, waliokaa mijini mwa Yuda, wakaleta pia zaka za ng'ombe na kondoo, na zaka za vitu vilivyowekwa wakfu, alivyowekewa Bwana, Mungu wao, wakaviweka chungu chungu. 7 Katika mwezi wa tatu wakaanza kuweka misingi ya hizo chungu, wakazimaliza katika mwezi wa saba. 8 Hata walipokuja Hezekia na wakuu, na kuziona zile chungu, wakamhimidi Bwana, na watu wake Israeli. 9 Ndipo Hezekia akaulizana na makuhani na Walawi katika habari ya hizo chungu. 10 Azaria kuhani mkuu, wa nyumba ya Sadoki, akamjibu, akasema, Tangu watu walipoanza kuleta matoleo nyumbani kwa Bwana, tumekula na kushiba, na kusaza tele; kwa kuwa Bwana amewabariki watu wake; na kilichosalia ndiyo akiba hii kubwa. 11 Ndipo Hezekia akaamuru kutengeneza vyumba nyumbani mwa Bwana; wakavitengeneza. 12 Wakayaingiza matoleo na zaka na vitu vilivyowekwa wakfu, kwa uaminifu; na juu yake Konania Mlawi alikuwa mkuu, na wa pili ni Shimei nduguye. 13 Na Yehieli, na Azaria, na Nahathi, na Asaheli, na Yerimothi, na Yozabadi, na Elieli, na Ismakia, na Mahathi, na Benaya, walikuwa wasimamizi chini ya mkono wa Konania na Shimei nduguye, kwa amri ya Hezekia mfalme, na Azaria mkuu wa nyumba ya Mungu. 14 Na Kore, mwana wa Imna, Mlawi, bawabu wa mlango wa mashariki, alizisimamia sadaka za hiari za Mungu; ili kugawa matoleo ya Bwana, navyo vitu vilivyokuwa vitakatifu sana. 15 Na chini yake walikuwa Edeni, na Minyamini, na Yeshua, na Shemaya, na Amaria, na Shekania, mijini mwa makuhani, kwa walivyoaminiwa, ili kuwagawia ndugu zao kwa zamu, wakuu na wadogo sawasawa; 16 zaidi ya wale waliohesabiwa kwa nasaba ya wanaume, wenye miaka mitatu na zaidi, kila mmoja aliyeingia nyumbani mwa Bwana, kama ilivyopasa kazi ya kila siku, kwa huduma zao katika malinzi yao, kwa kadiri ya zamu zao; 17 na wale waliohesabiwa kwa nasaba ya makuhani kufuata nyumba za baba zao, na Walawi, wenye umri wa miaka ishirini na zaidi, katika malinzi yao, kwa kadiri ya zamu zao; 18 na wale waliohesabiwa kwa nasaba ya wadogo wao wote, wake zao, na wana wao, na binti zao, katika kusanyiko lote; kwani kwa vile walivyoaminiwa, wakajitakasa katika utakatifu; 19 tena kwa ajili ya wana wa Haruni makuhani, waliokuwamo mashambani mwa malisho ya miji yao, mji kwa mji, kulikuwa na watu waliotajwa majina yao, ili kuwagawia sehemu wanaume wote miongoni mwa makuhani, na wote waliohesabiwa kwa nasaba miongoni mwa Walawi. 20 Na hivyo ndivyo alivyofanya Hezekia katika Yuda yote; akatenda yaliyo mema, na ya adili, na uaminifu, mbele za Bwana, Mungu wake. 21 Na katika kila kazi aliyoanza kwa utumishi wa nyumba ya Mungu, na kwa torati, na kwa amri, ili kumtafuta Mungu wake, aliifanya kwa moyo wake wote, akafanikiwa.

2 Mambo ya Nyakati 32

1 :Ikawa, baada ya mambo hayo, na uaminifu huo, Senakeribu, mfalme wa Ashuru, akaja, akaingia katika Yuda, akafanya marago juu ya miji yenye maboma, akadhania kwamba ataipata iwe yake. 2 Basi Hezekia, alipoona ya kuwa Senakeribu amekuja, na kuazimia kupigana na Yerusalemu, 3 akafanya shauri na wakuu wake, na mashujaa wake, kuzuia maji ya chemchemi zilizokuwa nje ya mji; nao wakamsaidia. 4 Wakakusanyika watu wengi, wakazizuia chemchemi zote, na kijito kilichopita kati ya nchi, wakisema, Kwa nini, wakifika wafalme wa Ashuru, waone maji mengi? 5 Akapiga moyo konde, akaujenga ukuta wote uliobomoka, akauinua sawa na minara, na ukuta wa pili nje, akaongeza nguvu ya Milo, katika mji wa Daudi, akafanya silaha na ngao tele. 6 Akaweka maakida wa vita juu ya watu, akawakusanya kwake uwandani penye lango la mji, akawafurahisha mioyo; akisema, 7 Iweni hodari, na wa moyo mkuu, msiogope, wala msifadhaike kwa sababu ya mfalme wa Ashuru, wala kwa majeshi yote walio pamoja naye; kwa maana yupo mkuu pamoja nasi kuliko aliye pamoja naye; 8 kwake upo mkono wa mwili; ila kwetu yupo Bwana, Mungu wetu, kutusaidia, na kutupigania mapigano yetu. Na watu wakayategemea maneno ya Hezekia, mfalme wa Yuda. 9 Na baada ya hayo Senakeribu mfalme wa Ashuru, akatuma watumishi wake waende Yerusalemu, (naye alikuwapo mbele ya Lakishi, na uwezo wake wote pamoja naye,) kwa Hezekia, mfalme wa Yuda, na kwa Yuda wote waliokuwako Yerusalemu, kusema, 10 Senakeribu, mfalme wa Ashuru, asema hivi, Mwatumainia nini hata mkae mkihusuriwa katika Yerusalemu? 11 Siye Hezekia anayewashawishi, mtolewe kufa kwa njaa na kwa kiu, akisema, Bwana, Mungu wetu, atatuokoa na mkono wa mfalme wa Ashuru? 12 Si yeye Hezekia huyo aliyeondoa mahali pake pa juu, na madhabahu zake, akawaamuru Yuda na Yerusalemu, akisema, Abuduni mbele ya madhabahu moja, na juu yake mtafukiza uvumba? 13 Je! Ninyi hamjui mimi na baba zangu tuliyowafanyia watu wote wa nchi? Je! Miungu ya mataifa wa nchi iliweza kuokoa kwa lo lote nchi zao na mkono wangu? 14 Ni yupi miongoni mwa miungu ya mataifa wale walioharibiwa kabisa na baba zangu, aliyeweza kuwaokoa watu wake na mkono wangu, hata Mungu wenu aweze kuwaokoa ninyi na mkono wangu? 15 Basi sasa asiwadanganye Hezekia, wala asiwashawishi kwa hayo, wala msimwamini; kwa kuwa hapana mungu wa taifa lo lote, wala wa ufalme wo wote, aliyeweza kuwaokoa watu wake na mkono wangu, au na mkono wa baba zangu; sembuse Mungu wenu atawaokoaje ninyi na mkono wangu? 16 Na watumishi wake wakazidi kusema juu ya Bwana Mungu, na juu ya Hezekia, mtumishi wake. 17 Tena akaandika waraka, kumtukana Bwana, Mungu wa Israeli, na kumwambia, akisema, Kama vile miungu ya mataifa wa nchi isivyowaokoa watu wao na mkono wangu, vivyo hivyo Mungu wa Hezekia hatawaokoa watu wake na mkono wangu. 18 Wakawalilia kwa sauti kuu, kwa lugha ya Kiyahudi, watu wa Yerusalemu waliokuwako ukutani ili kuwaogofisha, na kuwafadhaisha; hata wapate kuutwaa mji. 19 Wakamnenea Mungu wa Yerusalemu, kana kwamba kuitaja miungu ya mataifa wa nchi, iliyo kazi ya mikono ya watu. 20 Na kwa ajili ya hayo Hezekia mfalme, na Isaya nabii, mwana wa Amozi, wakaomba, wakalia hata mbinguni. 21 Naye Bwana akatuma malaika aliyewakatia mbali mashujaa wote, na majemadari, na maakida, matuoni mwa mfalme wa Ashuru. Basi akarudia nchi yake mwenye haya ya uso. Naye alipoingia nyumbani mwa mungu wake, wale waliotoka viunoni mwake mwenyewe wakamwangamiza humo kwa upanga. 22 Ndivyo Bwana alivyomwokoa Hezekia, na wenyeji wa Yerusalemu, na mkono wa Senakeribu, mfalme wa Ashuru, na mikononi mwa wote, akawaongoza pande zote. 23 Watu wengi walimletea Bwana zawadi huko Yerusalemu, na vitu vya thamani kwa Hezekia, mfalme wa Yuda; hata yeye akatukuka tangu wakati ule machoni pa mataifa yote. 24 Katika siku hizo Hezekia akaugua akawa katika hatari ya kufa; akamwomba Bwana; naye akasema naye, akampa ishara. 25 Walakini kadiri alivyofadhiliwa Hezekia hakumrudishia vivyo; kwa kuwa moyo wake ulitukuka; kwa hiyo ikawako hasira juu yake, na juu ya Yuda na Yerusalemu. 26 Hata hivyo Hezekia akajinyenyekeza kwa ajili ya huku kutukuka kwa moyo wake, yeye na wenyeji wa Yerusalemu, hata haikuwajia hasira ya Bwana siku za Hezekia. 27 Naye Hezekia akawa na mali nyingi mno na heshima; akajifanyizia hazina za fedha, na za dhahabu, na za vito, na za manukato, na za ngao, na za namna zote za vyombo vya thamani; 28 ghala pia za mazao ya nafaka na mvinyo na mafuta; na malisho ya wanyama wa namna zote, na makundi mazizini. 29 Tena akajifanyizia miji, na mali za kondoo na ng'ombe kwa wingi; maana Mungu alimtajirisha sana sana. 30 Naye huyo Hezekia ndiye aliyezuia chemchemi ya juu ya maji ya Gihoni, akayaleta chini moja kwa moja upande wa magharibi wa mji wa Daudi. Akafanikiwa Hezekia katika kazi zake zote. 31 Walakini kwa habari ya wajumbe wa wakuu wa Babeli, waliotuma kwake kuuliza ajabu iliyofanywa katika nchi, Mungu akamwacha, ili amjaribu, ili kwamba ayajue yote yaliyokuwamo moyoni mwake. 32 Basi mambo yote ya Hezekia yaliyosalia, na matendo yake mema, tazama, yameandikwa katika maono ya Isaya nabii, mwana wa Amozi, katika kitabu cha wafalme wa Yuda na Israeli. 33 Hezekia akalala na babaze, wakamzika mahali pa kupandia makaburi ya wana wa Daudi; nao Yuda wote na wenyeji wa Yerusalemu wakamfanyia heshima alipokufa. Na Manase mwanawe akatawala mahali pake.

2 Mambo ya Nyakati 33

1 Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka hamsini na mitano. 2 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, sawasawa na machukizo yote ya mataifa, aliowafukuza Bwana mbele ya wana wa Israeli. 3 Kwa maana akapajenga tena mahali pa juu alipopabomoa Hezekia babaye; akazisimamisha madhabahu za mabaali, akafanya na sanamu za maashera, akaabudu jeshi lote la mbinguni, na kulitumikia. 4 Akajenga madhabahu katika nyumba ya Bwana, napo ndipo alipopanena Bwana, Katika Yerusalemu litakuwako jina langu milele. 5 Akajenga madhabahu kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni katika nyua mbili za nyumba ya Bwana. 6 Tena akawapitisha wanawe motoni katika bonde la mwana wa Hinomu; akatazama bao, akabashiri, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa Bwana, hata kumkasirisha. 7 Akaiweka sanamu ya kuchonga aliyoifanya, katika nyumba ya Mungu ambayo Mungu alimwambia Daudi, na Sulemani mwanawe, Katika nyumba hii, na katika Yerusalemu, niliouchagua miongoni mwa kabila zote za Israeli, nitaliweka jina langu milele; 8 wala sitawaondoshea miguu tena Israeli katika nchi niliyowaagizia baba zenu; wakiangalia tu kutenda yote niliyowaamuru, yaani, torati yote, na sheria, na maagizo, niliyowaamuru kwa mkono wa Musa. 9 Basi Manase akawakosesha Yuda na wenyeji wa Yerusalemu, hata wakazidi kufanya mabaya kuliko mataifa, aliowaharibu Bwana mbele ya wana wa Israeli. 10 Naye Bwana akasema na Manase, na watu wake; wala wasiangalie. 11 Kwa hiyo Bwana akaleta juu yao maakida wa jeshi la mfalme wa Ashuru, waliomkamata Manase kwa minyororo, wakamfunga kwa pingu, wakamchukua mpaka Babeli. 12 Hata alipokuwa katika taabu, akamsihi Bwana, Mungu wake, akajinyenyekeza sana mbele za Mungu wa baba zake. 13 Akamwomba; naye akamtakabali, akayasikia maombi yake; akamrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake. Ndipo Manase akajua ya kwamba Bwana ndiye Mungu. 14 Hata baada ya hayo akaujengea mji wa Daudi ukuta wa nje, upande wa magharibi wa Gihoni, bondeni, hata kufika maingilio ya lango la samaki; akauzungusha Ofeli, akauinua juu sana; akaweka maakida mashujaa katika miji yote ya Yuda yenye maboma. 15 Akaiondoa miungu migeni, na hiyo sanamu nyumbani mwa Bwana, na madhabahu zote alizozijenga katika mlima wa nyumba ya Bwana, na Yerusalemu, akazitupa nje ya mji. 16 Akaijenga madhabahu ya Bwana, akatoa juu yake dhabihu za sadaka za amani, na za shukrani, akawaamuru Yuda wamtumikie Bwana, Mungu wa Israeli. 17 Lakini watu wakaendelea kutoa dhabihu katika mahali pa juu, ila wakamtolea Bwana, Mungu wao tu. 18 Basi mambo yote ya Manase yaliyosalia, na maombi yake kwa Mungu wake, na maneno ya waonaji walionena naye kwa jina la Bwana, Mungu wa Israeli, tazama, yameandikwa kati ya mambo ya wafalme wa Israeli. 19 Sala yake pia, na jinsi Mungu alivyomtakabali, na dhambi yake yote, na kosa lake, na mahali alipopajenga mahali pa juu, na kupasimamishia maashera na sanamu za kuchonga, kabla ya kujinyenyekeza; tazama, hayo yameandikwa katika tarehe ya Hozai. 20 Basi Manase akalala na babaze, wakamzika nyumbani mwake; na Amoni mwanawe akatawala mahali pake. 21 Amoni alikuwa na umri wa miaka ishirini na miwili alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka miwili. 22 Akafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, kama alivyofanya Manase babaye; Amoni akazitolea dhabihu sanamu zote alizozifanya Manase babaye, akazitumikia. 23 Wala hakujinyenyekeza mbele za Bwana, kama Manase babaye alivyojinyenyekeza; lakini huyo Amoni akaongeza makosa juu ya makosa. 24 Wakamfanyia fitina watumishi wake, wakamwua katika nyumba yake mwenyewe. 25 Lakini watu wa nchi wakawaua wote waliomfanyia fitina mfalme Amoni; watu wa nchi wakamfanya Yosia mwanawe awe mfalme badala yake.

2 Mambo ya Nyakati 34

1 Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala; akatawala miaka thelathini na mmoja huko Yerusalemu. 2 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, akaziendea njia za Daudi babaye, asigeuke kwa kuume wala kwa kushoto. 3 Kwa kuwa katika mwaka wa nane wa kutawala kwake, naye akali mchanga, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babaye; hata katika mwaka wa kumi na mbili akaanza kusafisha Yuda na Yerusalemu kwa kuondoa mahali pa juu, na kwa kuondoa maashera, na sanamu za kuchora, nazo za kusubu. 4 Wakazibomoa madhabahu za mabaali machoni pake; na sanamu za jua, zilizoinuliwa juu yake, akazikata-kata; na maashera, na sanamu za kuchonga, nazo za kusubu, akazivunja-vunja, akaziponda kuwa mavumbi, akayamimina juu ya makaburi ya hao waliozichinjia dhabihu. 5 Akaiteketeza mifupa ya makuhani madhabahuni mwao, akasafisha Yuda na Yerusalemu. 6 Na katika miji ya Manase, na Efraimu, na Simeoni, mpaka Naftali, akafanya vile vile; na katika maganjo yake pande zote. 7 Akazibomoa madhabahu, akaponda-ponda maashera na sanamu kuwa mavumbi, akazikata-kata sanamu zote za jua katika nchi yote ya Israeli, kisha akarejea Yerusalemu. 8 Hata katika mwaka wa kumi na nane wa kutawala kwake, alipokwisha kuisafisha nchi, na nyumba, akamtuma Shafani, mwana wa Azalia, na Maaseya, akida wa mji, na Yoa, mwana wa Yoahazi, mwandishi wa tarehe, waitengeneze nyumba ya Bwana, Mungu wake. 9 Wakamjia Hilkia kuhani mkuu, wakampa fedha, iliyoletwa nyumbani mwa Mungu, waliyoikusanya Walawi, wangoje mlango, mikononi mwa Manase na Efraimu, na mabaki yote ya Israeli, na Yuda yote na Benyamini, na wenyeji wa Yerusalemu. 10 Wakaitia mikononi mwa watenda kazi walioisimamia nyumba ya Bwana; na hao mafundi waliotenda kazi nyumbani mwa Bwana wakaitoa kwa kuitengeneza na kuifanya upya nyumba; 11 wakawapa maseremala na waashi, ili wanunue mawe ya kuchonga, na miti ya kuungia, na kuifanyiza boriti kwa nyumba zile walizoziharibu wafalme wa Yuda. 12 Nao watu wakatenda kazi kwa uaminifu; na wasimamizi wao walikuwa Yahathi na Obadia, Walawi, wa wana wa Merari; na Zekaria na Meshulamu, wa wana wa Wakohathi, ili kuihimiza kazi; na wengine katika Walawi, wote waliokuwa wastadi wa kupiga vinanda. 13 Tena walikuwa juu ya wachukuzi wa mizigo, wakawahimiza wote waliotenda kazi ya huduma yo yote; na miongoni mwa Walawi kulikuwa na waandishi, na wasimamizi, na mabawabu. 14 Nao walipotoa ile fedha iliyoletwa nyumbani mwa Bwana, Hilkia kuhani akakiona kitabu cha torati ya Bwana iliyotolewa kwa mkono wa Musa. 15 Akajibu Hilkia akamwambia Shafani mwandishi, Kitabu cha torati nimekiona nyumbani mwa Bwana. Hilkia akampa Shafani kile kitabu. 16 Shafani akampelekea mfalme hicho kitabu, tena akampasha mfalme habari, akisema, Yote waliyokabidhiwa watumishi wako, wayafanya. 17 Nao wameimimina fedha iliyoonekana nyumbani mwa Bwana, nayo wameitia mikononi mwa wasimamizi, na mikononi mwa watenda kazi. 18 Shafani mwandishi akamweleza mfalme, akisema, Hilkia kuhani amenipa kitabu. Shafani akasoma ndani yake mbele ya mfalme. 19 Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya torati, aliyararua mavazi yake. 20 Mfalme akawaamuru Hilkia, na Ahikamu, mwana wa Shafani, na Abdoni, mwana wa Mika, na Shafani mwandishi, na Asaya, mtumishi wa mfalme, kusema, 21 Nendeni, mkamwulize Bwana kwa ajili yangu, na kwa hao waliosalia wa Israeli na wa Yuda, katika habari za maneno ya kitabu kilichoonekana; maana ghadhabu ya Bwana ni nyingi iliyomwagika juu yetu, kwa sababu baba zetu hawakulishika neno la Bwana, kutenda sawasawa na yote yaliyoandikwa kitabuni humo. 22 Basi Hilkia, na hao waliotumwa na mfalme, wakamwendea Hulda nabii mke, mkewe Shalumu, mwana wa Tohathi, mwana wa Hasra, mtunza mavazi; (naye alikuwa akikaa Yerusalemu katika mtaa wa pili); wakasema naye kama hayo. 23 Akawaambia, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Mwambieni mtu huyo aliyewatuma kwangu, 24 Bwana asema hivi, Angalia, nitaleta mabaya juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, laana zote zilizoandikwa katika kitabu hicho walichokisoma mbele ya mfalme wa Yuda; 25 kwa sababu wameniacha mimi, na kuifukizia uvumba miungu mingine, ili wanikasirishe mimi kwa matendo yote ya mikono yao; kwa hiyo ghadhabu yangu imemwagika juu ya mahali hapa, wala isizimike. 26 Lakini mfalme wa Yuda, aliyewatuma kumwuliza Bwana, mtamwambia hivi, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Kwa habari ya maneno uliyoyasikia, 27 kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe umejinyenyekeza mbele ya Mungu, uliposikia maneno yake juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, ukajinyenyekeza mbele zangu, na kuyararua mavazi yako, na kulia mbele zangu; mimi nami nimekusikia, asema Bwana. 28 Tazama, nitakukusanya kwa baba zako, nawe utawekwa kaburini mwako kwa amani, wala macho yako hayataona mabaya yote nitakayoyaleta juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao. Basi wakamrudishia mfalme habari. 29 Ndipo mfalme akapeleka wajumbe, akawakusanya wazee wote wa Yuda na Yerusalemu. 30 Akapanda mfalme nyumbani kwa Bwana, na watu wote wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, na makuhani na Walawi, na watu wote, wakubwa kwa wadogo; naye akasoma masikioni mwao maneno yote ya kitabu cha agano kilichoonekana nyumbani mwa Bwana. 31 Akasimama mfalme mahali pake, akafanya agano mbele za Bwana, kumfuata Bwana, na kuzishika amri zake, na shuhuda zake, na sheria zake, kwa moyo wake wote, na kwa roho yake yote, kuyatenda maneno ya agano yaliyoandikwa kitabuni humo. 32 Akawafanya wote walioonekana katika Yerusalemu na Benyamini walikubali. Na wenyeji wa Yerusalemu wakafanya sawasawa na agano la Mungu, Mungu wa baba zao. 33 Naye Yosia akayaondolea mbali machukizo yote katika nchi zote zilizokuwa milki ya wana wa Israeli, akawafanya wote walioonekana katika Israeli kutumika, naam, wamtumikie Bwana, Mungu wao. Siku zake zote hawakuacha kumfuata Bwana, Mungu wa baba zao.

2 Mambo ya Nyakati 35

1 Naye Yosia akamfanyia Bwana pasaka huko Yerusalemu; wakachinja pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza. 2 Akawasimamisha makuhani katika malinzi yao, akawatia moyo kufanya utumishi wa nyumba ya Bwana. 3 Akawaambia Walawi, waliowafundisha Israeli wote, waliotakasika kwa Bwana, Wekeni sanduku takatifu katika nyumba aliyoijenga Sulemani, mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli; hamtakuwa tena na mzigo mabegani; sasa mtumikieni Bwana, Mungu wenu, na watu wake Israeli. 4 Mkajiweke tayari kwa kadiri ya nyumba za baba zenu, kwa zamu zenu, kama alivyoandika Daudi mfalme wa Israeli, na kama alivyoandika Sulemani mwanawe. 5 Mkasimame katika patakatifu, kama walivyogawanyika ndugu zenu, wana wa watu, kufuata nyumba za mababa, kadiri ya mgawanyiko wa kila nyumba ya baba, ya Walawi. 6 Mkachinje pasaka, mkajitakase, mkawatengenezee ndugu zenu, kutenda sawasawa na neno la Bwana kwa mkono wa Musa. 7 Tena Yosia akawapa wana wa watu, matoleo ya makundi, wana-kondoo na wana-mbuzi, yote yawe kwa ajili ya matoleo ya pasaka, wote waliokuwako, wakipata thelathini elfu, na ng'ombe elfu tatu; hao walitoka katika mali za mfalme. 8 Na wakuu wake wakawapa watu, na makuhani na Walawi matoleo ya hiari. Hilkia na wana na Yehieli, wakubwa wa nyumba ya Mungu, wakawapa makuhani, kuwa matoleo ya pasaka, wana-kondoo elfu mbili na mia sita, na ng'ombe mia tatu. 9 Konania naye, na Shemaya, na Nethaneli, ndugu zake, na Hashabia, na Yeieli, na Yozabadi, wakuu wa Walawi, wakawapa Walawi, kuwa matoleo ya pasaka, wana-kondoo elfu tano, na ng'ombe mia tano. 10 Hivyo huduma ikatengenezwa, wakasimama makuhani mahali pao, na Walawi kwa zamu zao, kama alivyoamuru mfalme. 11 Wakachinja pasaka, nao makuhani wakamimina damu waliyopokea mikononi mwao, Walawi wakachuna. 12 Wakaziondoa sadaka za kuteketezwa, wawape wana wa watu, kama walivyogawanyika kufuata nyumba za mababa, ili wamtolee Bwana, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Musa. Nao ng'ombe wakawafanya vivyo hivyo. 13 Wakaioka moto pasaka kama ilivyo sheria; wakatokosa matoleo matakatifu vyunguni, na masufuriani, na makaangoni, wakawachukulia upesi wana wa watu wote. 14 Baadaye wakajiandalia wenyewe, na makuhani; kwa sababu makuhani, wana wa Haruni, walikuwa na kazi ya kutoa sadaka za kuteketezwa, na mafuta hata usiku; kwa hiyo Walawi wakajiandalia wenyewe, na makuhani, wana wa Haruni. 15 Nao waimbaji, wana wa Asafu wakasimama mahali pao, kama alivyoamuru Daudi, na Asafu, na Hemani, na Yeduthuni mwonaji wa mfalme; nao mabawabu walikuwa katika kila lango; hawakuhitaji kuondoka katika huduma yao, kwa kuwa ndugu zao Walawi wakawaandalia. 16 Basi huduma yote ya Bwana ikatengenezwa siku ile ile, kuifanya pasaka, na kutoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu ya Bwana, kama alivyoamuru mfalme Yosia. 17 Wana wa Israeli waliokuwapo wakafanya pasaka wakati ule, na sikukuu ya mikate isiyochachwa muda wa siku saba. 18 Wala haikufanyika pasaka kama ile katika Israeli tangu siku za nabii Samweli; wala wafalme wa Israeli hawakufanya hata mmoja wao pasaka kama ile Yosia aliyoifanya, pamoja na makuhani, na Walawi, na Yuda wote na Israeli waliokuwapo, na wenyeji wa Yerusalemu. 19 Katika mwaka wa kumi na nane wa kutawala kwake Yosia ikafanyika pasaka hiyo. 20 Baada ya hayo yote, alipokwisha Yosia kulitengeneza hekalu, Neko, mfalme wa Misri, akakwea ili kupigana Karkemishi karibu na Frati; naye Yosia akatoka juu yake. 21 Lakini yeye akatuma kwake wajumbe, kusema, Ni nini niliyo nayo mimi na wewe, Ee mfalme wa Yuda? Sikuja juu yako leo, lakini juu ya nyumba niliyo na vita nayo; naye Mungu ameniamuru nifanye haraka; acha basi kumpinga Mungu, aliye pamoja nami, asikuharibu. 22 Walakini Yosia hakukubali kumgeuzia uso mbali, akajibadilisha apate kupigana naye, asiyasikilize maneno ya Neko, yaliyotoka kinywani kwa Mungu, akaja kupigana bondeni mwa Megido. 23 Nao wapiga upinde wakampiga Yosia; naye mfalme akawaambia watumishi wake, Niondoeni; kwani nimejeruhiwa sana. 24 Basi watumishi wake wakamtoa garini, wakamtia katika gari la pili alilokuwa nalo, wakamleta Yerusalemu; naye akafa, akazikwa makaburini mwa babaze. Wakamlilia Yosia Yuda wote na Yerusalemu. 25 Naye Yeremia akamlilia Yosia; na waimbaji wote waume kwa wake wakamtaja Yosia katika maombolezo yao, hata leo; hata wakayafanya kuwa ada kwa Israeli; nayo, tazama, yameandikwa katika maombolezo. 26 Basi mambo yote ya Yosia yaliyosalia, na matendo yake mema, sawasawa na yote yaliyoandikwa katika torati ya Bwana, 27 na mambo yake, ya kwanza na ya mwisho, tazama, yameandikwa katika kitabu cha wafalme wa Israeli na Yuda.

2 Mambo ya Nyakati 36

1 Watu wa nchi wakamtwaa Yehoahazi mwana wa Yosia, wakamtawaza awe mfalme katika Yerusalemu badala ya babaye. 2 Yehoahazi alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitatu alipoanza kutawala; akatawala huko Yerusalemu miezi mitatu. 3 Naye mfalme wa Misri akamwondoa katika Yerusalemu, akaitoza nchi talanta mia za fedha, na talanta moja ya dhahabu. 4 Mfalme wa Misri akamtawaza Eliakimu nduguye awe mfalme juu ya Yuda na Yerusalemu, akambadilisha jina lake kuwa Yehoyakimu. Neko akamtwaa Yehoahazi nduguye, akamchukua mpaka Misri. 5 Yehoyakimu alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka kumi na mmoja; akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, Mungu wake. 6 Juu yake akakwea Nebukadreza, 7 Nebukadreza akachukua baadhi ya vyombo vya nyumba ya Bwana mpaka Babeli, akavitia katika hekalu lake huko Babeli. 8 Basi mambo yote ya Yehoyakimu yaliyosalia, na machukizo yake aliyoyafanya, nayo yaliyoonekana kwake, tazama, yameandikwa katika kitabu cha wafalme wa Israeli na Yuda; na Yekonia 9 Yekonia alikuwa na umri wa miaka kumi na minane alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miezi mitatu na siku kumi; akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana. 10 Mwaka ulipokwisha, Nebukadreza akatuma wajumbe, akamchukua mpaka Babeli; pamoja na vyombo vya thamani vya nyumba ya Bwana; akamtawaza Sedekia nduguye awe mfalme juu ya Yuda na Yerusalemu. 11 Sedekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja, alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka kumi na mmoja; 12 akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, Mungu wake; wala hakujinyenyekesha mbele ya Yeremia nabii aliponena kwa kinywa cha Bwana. 13 Tena akamwasi mfalme Nebukadreza, aliyemwapisha kwa Mungu; lakini akajifanyia shingo ngumu, akajitia moyo nguvu asimgeukie Bwana, Mungu wa Israeli. 14 Na zaidi ya hayo wakuu wote wa makuhani, na watu, wakakosa mno sawasawa na machukizo yote ya mataifa; wakainajisi nyumba ya Bwana aliyoitakasa katika Yerusalemu. 15 Naye Bwana, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; 16 lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya Bwana juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya. 17 Kwa hiyo akaleta juu yao mfalme wa Wakaldayo, aliyewaua vijana wao kwa upanga nyumbani mwa patakatifu pao, asiwahurumie kijana wala mwanamwali, mzee wala mkongwe; akawatia wote mkononi mwake. 18 Na vyombo vyote vya nyumba ya Mungu, vikubwa kwa vidogo, na hazina za nyumba ya Bwana, na hazina za mfalme, na za wakuu wake; vyote pia akavileta Babeli. 19 Wakaiteketeza nyumba ya Mungu, wakaubomoa ukuta wa Yerusalemu, wakayateketeza kwa moto majumba yake yote, wakaviharibu vyombo vyake vyote vya thamani. 20 Na wale waliookoka na upanga akawachukua mpaka Babeli; wakamtumikia yeye na wanawe hata kulipoingia milki ya Uajemi; 21 ili kulitimiza neno la Bwana kwa kinywa cha Yeremia, hata nchi itakapofurahia sabato zake; kwa maana siku zote ilipokaa ukiwa ilishika sabato, kutimiza miaka sabini. 22 Ikawa katika mwaka wa kwanza wa Koreshi, mfalme wa Uajemi, ili kwamba neno la Bwana alilolisema kwa kinywa cha Yeremia lipate kutimizwa, Bwana akamwamsha roho yake Koreshi, mfalme wa Uajemi, hata akapiga mbiu katika ufalme wake wote, akaiandika pia, akisema, 23 Koreshi, mfalme wa Uajemi asema hivi; Bwana, Mungu wa mbinguni, amenipa falme zote za dunia; naye ameniagiza nimjengee nyumba katika Yerusalemu, ulioko Yuda. Basi kila mtu katika ninyi nyote mlio watu wake, Bwana, Mungu wake, na awe pamoja naye, na akwee.

Ezra 1

1 Ikawa katika mwaka wa kwanza wa Koreshi, mfalme wa Uajemi, ili kwamba neno la Bwana alilolisema kwa kinywa cha Yeremia lipate kutimizwa, Bwana akamwamsha roho yake Koreshi, mfalme wa Uajemi, hata akapiga mbiu katika ufalme wake wote, akaiandika pia, akisema, 2 Koreshi, mfalme wa Uajemi asema hivi; 3 Basi kila mtu katika ninyi nyote mlio watu wake, Bwana, Mungu wake, na awe pamoja naye, na akwee mpaka Yerusalemu, ulioko Yuda, akaijenge nyumba ya Bwana, Mungu wa Israeli, (yeye ndiye Mungu), iliyoko Yerusalemu. 4 Na mtu awaye yote aliyesalia mahali po pote akaapo hali ya ugeni, na asaidiwe na watu wa mahali pake, kwa fedha, na dhahabu, na mali, na wanyama, zaidi ya vitu vitolewavyo kwa hiari ya mtu, kwa ajili ya nyumba ya Mungu, iliyoko Yerusalemu. 5 Ndipo wakaondoka wakuu wa mbari za mababa, wa Yuda na Benyamini, na makuhani, na Walawi, naam, watu wote ambao Mungu amewaamsha roho zao kukwea, ili kuijenga nyumba ya Bwana, iliyoko Yerusalemu. 6 Na watu wote waliokaa karibu nao pande zote wakawatia nguvu mikono yao, kwa vyombo vya fedha, kwa dhahabu, kwa mali, na kwa wanyama, na vitu vya thamani, zaidi ya vile vilivyotolewa kwa hiari ya mtu. 7 Tena Koreshi, mfalme, alivitoa vyombo vya nyumba ya Bwana, alivyokuwa amevileta Nebukadreza toka Yerusalemu ,na kuvitia katika nyumba ya miungu yake. 8 Naam, vyombo vile ndivyo alivyovitoa Koreshi, mfalme wa Uajemi, kwa mkono wa Mithredathi, mtunza hazina; naye akavihesabu mbele ya Sheshbaza, mkuu wa Yuda. 9 Na hii ndiyo hesabu yake; sinia za dhahabu thelathini, sinia za fedha elfu, visu ishirini na kenda. 10 mabakuli ya dhahabu thelathini, mabakuli ya fedha ya namna ya pili mia nne na kumi, na vyombo vingine elfu. 11 Vyombo vyote vya dhahabu na vya fedha vilikuwa jumla yake elfu tano na mia nne. Hivyo vyote Sheshbaza akakwea navyo, hapo walipokwea wale wa uhamisho kutoka Babeli mpaka Yerusalemu.

Ezra 2

1 Basi hawa ndio wana wa wilaya, waliokwea kutoka katika ule uhamisho wa hao waliokuwa wamechukuliwa, ambao Nebukadneza, mfalme wa Babeli, aliwachukua mateka mpaka Babeli, nao wakarudi Yerusalemu na Yuda, kila mtu mjini kwake; 2 ndio hawa waliokuja pamoja na Zerubabeli, Yoshua, Nehemia, Seraya, Reelaya, Mordekai, Bilshani, Mispari, Bigwai, Rehumu, na Baana. Hii ndiyo hesabu ya wanaume wa watu wa Israeli; 3 wana wa Paroshi, elfu mbili mia moja sabini na wawili. 4 Wana wa Shefatia, mia tatu sabini na wawili. 5 Wana wa Ara, mia saba sabini na watano. 6 Wana wa Pahath-Moabu, wa wana wa Yeshua na Yoabu, elfu mbili mia nane na kumi na wawili. 7 Wana wa Elamu, elfu moja mia mbili hamsini na wanne. 8 Wana wa Zatu, mia kenda arobaini na watano. 9 Wana wa Zakai, mia saba na sitini. 10 Wana wa Binui, mia sita arobaini na wawili. 11 Wana wa Bebai, mia sita ishirini na watatu. 12 Wana wa Azgadi, elfu moja mia mbili ishirini na wawili. 13 Wana wa Adonikamu, mia sita sitini na sita. 14 Wana wa Bigwai, elfu mbili hamsini na sita. 15 Wana wa Adini, mia nne hamsini na wanne. 16 Wana wa Ateri, wa wana wa Hezekia, tisini na wanane. 17 Wana wa Besai, mia tatu ishirini na watatu. 18 Wana wa Harifu, mia moja na kumi na wawili. 19 Wana wa Hashumu, mia mbili ishirini na watatu. 20 Watu wa Gibeoni, tisini na watano. 21 Watu wa Bethlehemu, mia ishirini na watatu. 22 Watu wa Netofa, hamsini na sita. 23 Watu wa Anathothi, mia ishirini na wanane. 24 Watu wa Beth-Azmawethi, arobaini na wawili. 25 Watu wa Kiriath-yearimu, na Kefira, na Beerothi, mia saba arobaini na watatu. 26 Watu wa Rama na Geba, mia sita ishirini na mmoja. 27 Watu wa Mikmashi, mia moja ishirini na wawili. 28 Watu wa Betheli, na Ai, mia mbili ishirini na watatu. 29 Watu wa Nebo, hamsini na wawili. 30 Watu wa Magbishi, mia moja hamsini na sita. 31 Watu wa Elamu wa pili, elfu moja mia mbili hamsini na wanne. 32 Watu wa Harimu, mia tatu na ishirini. 33 Watu wa Lodi, na Hadidi, na Ono, mia saba ishirini na watano. 34 Watu wa Yeriko, mia tatu arobaini na watano. 35 Watu wa Senaa, elfu tatu mia sita na thelathini. 36 Makuhani; wana wa Yedaya, wa mbari ya Yeshua, mia kenda sabini na watatu. 37 Wana wa Imeri, elfu moja hamsini na wawili. 38 Wana wa Pashuri, elfu moja mia mbili arobaini na saba. 39 Wana wa Harimu, elfu moja na kumi na saba. 40 Walawi; wana wa Yeshua, na wana wa Kadmieli wa wana wa Hodavia, sabini na wanne. 41 Waimbaji; wana wa Asafu, mia moja ishirini na wanane. 42 Akina bawabu; wana wa Shalumu, wana wa Ateri, wana wa Talmoni, wana wa Akubu, wana wa Hatita, wana wa Shobai; jumla yao ni mia moja thelathini na kenda. 43 Wanethini; wana wa Siha, wana wa Hasufa, wana wa Tabaothi; 44 wana wa Kerosi, wana wa Siaha, wana wa Padoni; 45 wana wa Lebana, wana wa Hagaba, wana wa Akubu; 46 wana wa Hagabu, wana wa Salmai, wana wa Hanani; 47 wana wa Gideli, wana wa Gahari, wana wa Reaya; 48 wana wa Resini, wana wa Nekoda, wana wa Gazamu; 49 wana wa Uza, wana wa Pasea, wana wa Besai; 50 wana wa Asna, wana wa Meunimu, wana wa Nefusimu; 51 wana wa Bakbuki, wana wa Hakufa, wana wa Harhuri; 52 wana wa Basluthi, wana wa Mehida, wana wa Harsha; 53 wana wa Barkosi, wana wa Sisera, wana wa Tema; 54 wana wa Nesia, wana wa Hatifa. 55 Wa watumwa wa Sulemani; wana wa Sotai, wana wa Soferethi, wana wa Peruda; 56 wana wa Yaala, wana wa Darkoni, wana wa Gideli; 57 wana wa Shefatia, wana wa Hatili, wana wa Pokereth-Sebaimu, wana wa Amoni. 58 Wanethini wote, pamoja na watumwa wa Sulemani, walikuwa mia tatu tisini na wawili. 59 Na hawa ndio watu waliokwea kutoka Tel-mela, na Tel-harsha, na Kerubu, na Adani, na Imeri; walakini hawakuweza kuonyesha mbari za baba zao, wala kizazi chao, kwamba walikuwa wa Israeli; 60 wana wa Delaya, wana wa Tobia, wana wa Nekoda, mia sita hamsini na wawili. 61 Tena wa makuhani; wana wa Habaya, wana wa Hakosi, wana wa Barzilai, yule aliyeoa mmojawapo wa binti Barzilai, Mgileadi, akaitwa kwa jina lao. 62 Hao waliitafuta orodha yao miongoni mwa wale waliohesabiwa kwa nasaba, wasionekane; kwa hiyo walihesabiwa kuwa na unajisi. 63 Na huyo Tirshatha akawaambia wasile katika vitu vitakatifu sana ,hata atakaposimama kuhani mwenye urimu na Thumimu. 64 Basi hilo kusanyiko lote zima, jumla yake ilikuwa watu arobaini na mbili elfu na mia tatu na sitini, 65 tena, zaidi ya hao, kulikuwa na watumishi wao waume kwa wake, ambao walikuwa saba elfu, na mia tatu na thelathini na saba; nao walikuwa na waimbaji waume kwa wake mia mbili. 66 Farasi zao walikuwa mia saba thelathini na sita; nyumbu zao, mia mbili arobaini na watano; 67 ngamia zao, mia nne thelathini na watano; punda zao elfu sita, na mia saba na ishirini. 68 Na baadhi ya wakuu wa mbari za baba zao, hapo walipoifikilia nyumba ya Bwana, iliyoko Yerusalemu, walitoa mali kwa ukarimu kwa ajili ya nyumba ya Mungu, ili kuisimamisha mahali pake; 69 wakatoa kadiri walivyoweza, na kutia katika hazina ya kazi hiyo, darkoni za dhahabu sitini na moja elfu ,na nane za fedha elfu tano,na mavazi mia ya makuhani. 70 Hivyo makuhani, na Walawi, na baadhi ya watu, na waimbaji, na mabawabu, na Wanethini, wakakaa mijini mwao, naam, Israeli wote wakakaa mijini mwao.

Ezra 3

1 Hata ulipowadia mwezi wa saba, na wana wa Israeli walipokuwa katika miji yao, watu wakakusanyika pamoja huko Yerusalemu kama mtu mmoja. 2 Ndipo akasimama Yoshua, mwana wa Yosadaki, na ndugu zake makuhani, na Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na ndugu zake, nao wakaijenga madhabahu ya Mungu wa Israeli, ili kutoa sadaka za kuteketezwa juu yake, kama ilivyoandikwa katika torati ya Musa, mtu wa Mungu. 3 Wakaiweka madhabahu juu ya msingi wake; maana hofu imewashika kwa sababu ya watu wa nchi; wakamtolea Bwana sadaka za kuteketezwa juu yake, sadaka za kuteketezwa za asubuhi na jioni. 4 Wakaishika Sikukuu ya Vibanda, kama ilivyoandikwa, wakatoa sadaka za kuteketezwa za kila siku kwa hesabu yake, kama ilivyoagizwa, kama ilivyopasa kila siku; 5 na baadaye sadaka ya kuteketezwa ya daima, na za mwandamo wa mwezi, na za sikukuu za Bwana, zilizoamriwa na kuwekwa wakfu, na za kila mtu aliyemtolea Bwana sadaka kwa hiari yake. 6 Tangu siku ya kwanza ya mwezi wa saba walianza kumtolea Bwana sadaka za kuteketezwa, lakini msingi wa hekalu la Bwana ulikuwa haujawekwa bado. 7 Tena waliwapa waashi na maseremala fedha; wakawapa watu wa Sidoni, na watu wa Tiro, chakula, na vinywaji, na mafuta, ili walete mierezi kutoka Lebanoni mpaka Yafa kwa njia ya bahari, kwa kadiri walivyopewa ruhusa na Koreshi, mfalme wa Uajemi. 8 Hata mwaka wa pili wa kufika kwao nyumbani kwa Mungu, huko Yerusalemu, mwezi wa pili, Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na Yoshua, mwana wa Yosadaki, na ndugu zao wengine, makuhani na Walawi, na watu wote, waliotoka katika uhamisho na kufika Yerusalemu, wakaanza; nao wakawaweka Walawi, hao wenye miaka ishirini na waliozidi, ili kuisimamia kazi ya nyumba ya Bwana. 9 Ndipo wakasimama Yeshua, na wanawe na ndugu zake, Kadmieli, na wanawe, wana wa Hodavia, pamoja, ili kuwasimamia hao wafanyao kazi katika nyumba ya Mungu; wana wa Henadadi, pamoja na wana wao, na ndugu zao, Walawi. 10 Hata wajenzi walipouweka msingi wa hekalu la Bwana, wakawaweka makuhani, wamevaa mavazi yao, wenye baragumu, na Walawi, wana wa Asafu, wenye matoazi, ili wamhimidi Bwana, kama alivyoagiza Daudi, mfalme wa Israeli. 11 Wakaimbiana, wakimhimidi Bwana, na kumshukuru, wakasema, Kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake kwa Israeli ni za milele. Kisha watu wote wakapaza sauti zao, na kupiga kelele, walipomhimidi Bwana, kwa sababu msingi wa nyumba ya Bwana umekwisha kuwekwa. 12 Bali makuhani wengi, na Walawi, na wakuu wa mbari za mababa, waliokuwa wameiona nyumba ya kwanza, wakati msingi wa nyumba hii ulipowekwa mbele ya macho yao, walilia kwa sauti kuu; na watu wengi walipiga kelele za furaha; 13 hata watu wasiweze kupambanua kelele za furaha, na kelele za vilio vya watu; maana watu walipiga kelele kwa sauti kuu, na kelele zao zikasikilikana mbali sana.

Ezra 4

1 Basi adui za Yuda na Benyamini, waliposikia ya kuwa wana wa uhamisho wanamjengea Bwana, Mungu wa Israeli, hekalu, 2 wakamkaribia Zerubabeli, na wakuu wa mbari za mababa, wakawaambia, Na tujenge sisi nasi pamoja nanyi; kwa maana tunamtafuta Mungu wenu kama ninyi, nasi twamtolea dhabihu tangu zamani za Esar-hadoni, mfalme wa Ashuru, aliyetupandisha mpaka hapa. 3 Lakini Zerubabeli, na Yoshua, na wakuu wengine wa mbari za mababa katika Israeli, wakawaambia, Ninyi haiwahusu kushirikiana nasi katika kumjengea Mungu wetu nyumba; bali sisi wenyewe peke yetu tutamjengea Bwana, Mungu wa Israeli, nyumba, kama mfalme Koreshi, mfalme wa Uajemi, alivyotuamuru. 4 Ndipo watu wa nchi wakaidhoofisha mikono ya watu wa Yuda, wakawasumbua, walipokuwa wakijenga. 5 Wakawaajiri washauri juu yao, ili kuwapinga kusudi lao, siku zote za Koreshi, mfalme wa Uajemi, hata wakati wa kutawala kwake Dario, mfalme wa Uajemi. 6 Tena, wakati wa kutawala kwake Ahasuero, mwanzo wa kutawala kwake, watu wakaandika mashitaka juu ya wenyeji wa Yuda na Yerusalemu. 7 Na tena, katika siku za Artashasta, Mithredathi, na Tabeeli na mabaki ya wenziwe, wakimwandikia Artashasta, mfalme wa Uajemi, salamu za heri; na mwandiko wa waraka huo, ukaandikwa kwa herufi za Kiaramu, na kunenwa kwa lugha ya Kiaramu. 8 Nao Rehumu, Bwana shauri, na Shimshai, mwandishi, wakaandika waraka juu ya Yerusalemu kwa Artashasta, mfalme, kama hivi; 9 Rehumu, Bwana shauri, na Shimshai, mwandishi, na mabaki ya wenzao, makadhi wa Kiajemi na madiwani wa Kiajemi; na Waarkewi, Wababeli, Washushani, yaani, Waelami; 10 na mabaki ya mataifa, ambao Asur-bani-pali mkuu, mwenye heshima, aliwavusha, na kuwakalisha katika mji wa Samaria, na mahali penginepo, ng'ambo ya Mto; wakadhalika. 11 Hii ndiyo nakili ya waraka waliyompelekea mfalme Artashasta;watumishi wako,watu walio ng`ambo ya mto wakadhalika. 12 Ijulikane kwa mfalme ya kuwa Wayahudi, waliokwea kutoka kwako, wamefika kwetu Yerusalemu; nao wanaujenga ule mji mwasi, mbaya; wamemaliza kuta zake, na kuitengeneza misingi yake. 13 Basi, ijulikane kwa mfalme, ya kuwa mji huu ukijengwa, na kuta zake zikimalizika, hawatatoa kodi, wala ada, wala ushuru, na mwisho wake wafalme watapata hasara. 14 Na sisi, kwa kuwa tunakula chumvi ya nyumba ya mfalme, wala si wajibu wetu kumwona mfalme akivunjiwa heshima, basi tumetuma watu na kumwarifu mfalme. 15 Ili habari zitafutwe katika kitabu cha tarehe za baba zako; ndivyo utakavyopata kujua kwa kitabu cha tarehe ya kuwa mji huo ni mji mwasi, wenye kuwadhuru wafalme, na maliwali, na ya kuwa wenyeji wake wamefanya fitina katika mji huo zamani; ndiyo sababu mji huo ukaangamizwa. 16 Twamwarifu mfalme ya kuwa mji huo ukijengwa, na kuta zake zikimalizika, hutakuwa na sehemu ya nchi ng'ambo ya Mto. 17 Ndipo mfalme akapeleka majibu;Kwa Rehumu,Bwana shauri, na Shimshai,mwandishi na wenzao wengine waliokaa katika Samaria,na penginepo ng`ambo ya mto, Salamu; wakadharika. 18 Ule waraka mlionipelekea umesomwa mbele yangu, nami nikaelewa na maana yake. 19 Nikatoa amri, na watu wametafuta habari; ikaonekana ya kuwa mji huu zamani umefanya fitina juu ya wafalme, na ya kuwa uasi na fitina zimefanyika ndani yake. 20 Tena walikuwako wafalme wakuu juu ya Yerusalemu, waliotawala nchi yote iliyo ng'ambo ya Mto; wakapewa kodi, na ada, na ushuru. 21 Sasa toeni amri kuwakomesha watu hawa kazi yao, mji huu usijengwe, hata mimi nitakapotoa amri. 22 Tena jihadharini, msilegee katika jambo hili; kwa nini madhara yazidi, na wafalme wapate hasara? 23 Hata nakala ya waraka huo wa mfalme Artashasta uliposomwa mbele ya Rehumu, Bwana shauri, na Shimshai, mwandishi, na wenzao, wakaenda Yerusalemu upesi, kwa Wayahudi, wakawakomesha kwa nguvu na kwa kuwashurutisha. 24 Hivyo kazi ya nyumba ya Mungu iliyoko Yerusalemu ikakoma; nayo ikakoma hata mwaka wa pili wa kutawala kwake Dario, mfalme wa Uajemi.

Ezra 5

1 Basi manabii, Hagai nabii, na Zekaria mwana wa Ido, wakawafanyia unabii Wayahudi waliokuwako Yerusalemu na Yuda; waliwafanyia unabii kwa jina la Mungu wa Israeli. 2 Ndipo akaondoka Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na Yoshua, mwana wa Yosadaki, wakaanza kuijenga nyumba ya Mungu iliyoko Yerusalemu; na pamoja nao walikuwa manabii wa Mungu, wakiwasaidia. 3 Wakati ule ule Tatenai, liwali wa ng'ambo ya Mto, na Shethar-Bozenai, na wenzi wao, wakawajia, wakawaambia, Ni nani aliyewapa amri kuijenga nyumba hii, na kuumaliza ukuta huu? 4 Ndipo wakawauliza hivi, Majina ya watu wanaofanya ujenzi huu ni nani na nani? 5 Lakini jicho la Mungu lilikuwa likiwaelekea wazee wa Wayahudi, hao wasiwazuie, hata habari ile imfikilie Dario, ndipo jawabu litakapopatikana kwa waraka. 6 Hii ndiyo nakala ya waraka waliyompelekea mfalme Dario; na Tatenai, liwali wa ng'ambo ya Mto, na Shethar-Bozenai, na wenzake wa Kiajemi, waliokuwako huko ng'ambo ya Mto, 7 walimpelekea waraka nao; na maneno haya yakaandikwa ndani yake; Kwa Dario, mfalme; Salamu sana. 8 Na ajue mfalme ya kuwa sisi tuliingia nchi ya Yuda, tukafika kunako nyumba ya Mungu mkuu, iliyojengwa kwa mawe makubwa, na miti imetiwa katika kuta zake, na kazi hii inaendelea kwa bidii, na kusitawi katika mikono yao. 9 Ndipo tukawauliza wale wazee, tukawaambia hivi, Ni nani aliyewapa amri kuijenga nyumba hii, na kuumaliza ukuta huu? 10 Tukawauliza pia majina yao, ili kukuarifu wewe, tupate kuandika majina ya watu waliokuwa wakubwa wao. 11 Wakatujibu hivi, wakasema, Sisi tu watumishi wa Mungu wa mbingu na nchi, nasi tunaijenga nyumba iliyojengwa zamani sana, yapata miaka mingi, ambayo mfalme mkuu wa Israeli aliijenga na kuimaliza. 12 Lakini hapo baba zetu walipomkasirisha Mungu wa mbingu na nchi, hata akaghadhibika, akawatia katika mkono wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, Mkaldayo, naye ndiye aliyeiharibu nyumba hii, akawachukua watu mateka mpaka Babeli. 13 Lakini katika mwaka wa kwanza wa Koreshi, mfalme wa Babeli, Koreshi, mfalme, alitoa amri ijengwe tena nyumba ya Mungu. 14 Na vyombo vya dhahabu na fedha, vya nyumba ya Mungu, alivyovitoa Nebukadreza katika hekalu lililokuwako Yerusalemu, na kuviingiza katika hekalu la Babeli, vyombo hivyo mfalme Koreshi alivitoa katika hekalu la Babeli, akakabidhiwa mtu, jina lake Sheshbaza, ambaye alikuwa amemfanya liwali; 15 naye akamwambia, Chukua vyombo hivi, uende, ukavitie katika hekalu lililoko Yerusalemu, na nyumba ya Mungu na ijengwe mahali pake. 16 Ndipo ye yule Sheshbaza alipokuja, akaupiga msingi wa nyumba ya Mungu iliyoko Yerusalemu; na tangu wakati ule hata leo imekuwa ikijengwa, wala bado haijamalizika. 17 Basi, sasa, mfalme akiona vema, watu na watafute katika nyumba ya hazina ya mfalme, iliyoko huko Babeli, kama ni kweli ya kuwa mfalme Koreshi alitoa amri kuijenga nyumba hiyo ya Mungu katika Yerusalemu, na mfalme akatuletee habari ya mapenzi yake katika jambo hili.

Ezra 6

1 Ndipo mfalme Dario akatoa amri, na watu wakatafuta katika nyumba ya vyuo vya tarehe, hapo akiba zilipowekwa katika Babeli. 2 Na chuo kimoja kilipatikana huko Akmetha, katika nyumba ya mfalme iliyo katika wilaya ya Umedi, na ndani yake maneno haya yameandikwa ili yakumbukwe. 3 Katika mwaka wa kwanza wa mfalme Koreshi, mfalme Koreshi alitoa amri, Kwa habari ya nyumba ya Mungu huko Yerusalemu, nyumba hiyo na ijengwe, mahali watoapo dhabihu, na misingi yake ipigwe na kufanywa imara sana; kuinuka kwake kuwe mikono sitini, na upana wake mikono sitini; 4 ziwepo safu tatu za mawe makubwa, na safu moja ya miti mipya; gharama zake zitolewe katika nyumba ya mfalme. 5 Na vyombo vya dhahabu na fedha, vya nyumba ya Mungu, ambavyo mfalme Nebukadreza alivitoa katika nyumba ya Mungu, iliyoko Yerusalemu, akavileta mpaka Babeli, na virudishwe, vikaingizwe tena katika hekalu lililoko Yerusalemu, kila kimoja mahali pake, na wewe uvitie katika nyumba ya Mungu. 6 Basi sasa ninyi, Tatenai, liwali wa ng'ambo ya Mto, na Shethar-Bozenai, na hao wenzi wenu wa Kiajemi, mlio ng'ambo ya Mto, jitengeni na mahali pale; 7 iacheni kazi hii ya nyumba ya Mungu, msiizuie; waacheni liwali wa Wayahudi, na wazee wa Wayahudi, waijenge nyumba hii ya Mungu mahali pake. 8 Tena, natoa amri kuwaagiza ninyi mtakayowatendea wazee hao wa Wayahudi, kwa kazi hii ya kuijenga nyumba ya Mungu; katika mali ya mfalme, yaani, katika kodi za nchi iliyo ng'ambo ya Mto, watu hao wapewe gharama zote kwa bidii, ili wasizuiliwe. 9 Na kila kitu wanachokihitaji, katika ng'ombe wachanga, na kondoo waume, na wana-kondoo, kwa sadaka za kuteketezwa watakazomtolea Mungu wa mbinguni, na ngano, na chumvi, na divai, na mafuta, kama makuhani walioko Yerusalemu watakavyosema, na wapewe vitu hivyo vyote siku kwa siku, msikose kuwapa; 10 wapate kumtolea Mungu wa mbinguni sadaka zenye harufu nzuri, na kumwombea mfalme, na wanawe, wapate uzima. 11 Pia nimetoa amri kwamba, mtu awaye yote atakayelibadili neno hili, boriti na itolewe katika nyumba yake, akainuliwe na kutungikwa juu yake; tena nyumba yake ikafanywe jaa kwa ajili ya neno hili. 12 Na Mungu huyu, aliyelifanya jina lake likae pale, na aangamize wafalme wote, na watu wote, watakaonyosha mikono yao kulibadili neno hili, na kuiharibu nyumba hii ya Mungu, iliyoko Yerusalemu. Mimi, Dario, nimetoa amri; na ifanyike kwa bidii nyingi. 13 Ndipo Tatenai, liwali wa ng'ambo ya Mto, na Shethar-Bozenai, na wenzi wao, wakafanya hayo kwa bidii, kwa sababu mfalme Dario alikuwa ametuma watu kwao. 14 Nao wazee wa Wayahudi wakajenga, wakafanikiwa, kwa msaada wa kuhubiri kwao Hagai nabii, na Zekaria mwana wa Ido. Wakajenga, wakaimaliza kazi yao, kwa maagizo ya Mungu wa Israeli, na kwa amri ya Koreshi, na Dario, na Artashasta mfalme wa Uajemi. 15 Nyumba hiyo ikamalizika siku ya tatu ya mwezi Adari, katika mwaka wa sita wa kutawala kwake mfalme Dario. 16 Na wana wa Israeli, na makuhani na Walawi, na watu wengine katika hao waliohamishwa, wakaiweka wakfu nyumba ya Mungu kwa furaha. 17 Na katika kuiweka wakfu nyumba ya Mungu, wakatoa sadaka, ng'ombe mia, na kondoo waume mia mbili, na wana-kondoo mia nne; tena wakatoa mbuzi waume kumi na wawili, kuwa sadaka ya dhambi kwa ajili ya Israeli wote, kwa hesabu ya kabila za Israeli. 18 Wakawaweka makuhani katika kura zao, wakawaweka na Walawi katika zamu zao, kwa ajili ya huduma ya Mungu, iliyokuwako Yerusalemu; vile vile kama vilivyoandikwa katika chuo cha Musa. 19 Kisha, wana wa uhamisho wakaifanya Pasaka, mwezi wa kwanza siku ya kumi na nne ya mwezi. 20 Kwa maana makuhani na Walawi walikuwa wamejitakasa wote pamoja; wote walikuwa hali ya tohara; wakachinja Pasaka kwa ajili ya wana wote wa uhamisho, na kwa ajili ya ndugu zao makuhani, na kwa ajili ya nafsi zao. 21 Wana wa Israeli wakaila, wale waliorudi kuitoka nchi ya uhamisho wao, na watu wote ambao pamoja nao wamejitenga na uchafu wa taifa za nchi, ili kumtaka Bwana, Mungu wa Israeli, 22 wakaifanya sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu kwa furaha, kwa muda wa siku saba; kwa kuwa Bwana amewafurahisha, na kumgeuza moyo mfalme wa Ashuru, awaelekee, ili awatie nguvu mikono yao katika kazi hiyo ya nyumba ya Mungu, Mungu wa Israeli.

Ezra 7

1 Ikawa baada ya mambo hayo, wakati wa kutawala kwake Artashasta, mfalme wa Uajemi, Ezra, mwana wa Seraya, mwana wa Azaria, mwana wa Hilkia, 2 mwana wa Shalumu, mwana wa Sadoki, mwana wa Ahitubu, 3 mwana wa Amaria, mwana wa Azaria, mwana wa Merayothi, 4 mwana wa Zerahia, mwana wa Uzi, mwana wa Buki, 5 mwana wa Abishua, mwana wa Finehasi, mwana wa Eleazari, mwana wa Haruni, kuhani mkuu; 6 huyo Ezra akakwea kutoka Babeli; naye alikuwa mwandishi mwepesi katika sheria ya Musa, aliyokuwa ameitoa Bwana, Mungu wa Israeli; naye mfalme akamjalia matakwa yake yote, kama mkono wa Bwana, Mungu wake, ulivyokuwa pamoja naye. 7 Nao wakakwea baadhi ya wana wa Israeli, na wa makuhani, na wa Walawi, na waimbaji, na mabawabu, na Wanethini, ili kwenda Yerusalemu, katika mwaka wa saba wa mfalme Artashasta. 8 Naye Ezra akafika Yerusalemu mwezi wa tano katika mwaka wa saba wa huyo mfalme. 9 Maana alianza kukwea kutoka Babeli siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, naye akafika Yerusalemu siku ya kwanza ya mwezi wa tano, kama mkono mwema wa Mungu wake ulivyokuwa pamoja naye. 10 Kwa maana huyo Ezra alikuwa ameuelekeza moyo wake kuitafuta sheria ya Bwana, na kuitenda, na kufundisha maagizo na hukumu katika Israeli. 11 Basi hii ndiyo nakala ya waraka, mfalme Artashasta aliyompa Ezra, kuhani, mwandishi, naam, mwandishi wa maneno ya amri za Bwana, na wa sheria zake alizowapa Israeli. 12 Artashasta, mfalme wa wafalme, kwa Ezra, kuhani, mwandishi wa torati ya Mungu wa mbinguni, salamu kamili; wakadhalika. 13 Natoa amri ya kwamba wote walio wa watu wa Israeli, na makuhani wao, na Walawi, katika ufalme wangu, wenye nia ya kwenda Yerusalemu kwa hiari yao wenyewe, waende pamoja nawe. 14 Kwa kuwa umetumwa na mfalme, na washauri wake saba, ili kuuliza habari za Yuda na Yerusalemu, kwa sheria ya Mungu wako iliyo mkononi mwako; 15 na kuichukua fedha na dhahabu, ambayo mfalme, na washauri wake, kwa hiari yao, wamemtolea Mungu wa Israeli, akaaye Yerusalemu; 16 na fedha yote na dhahabu utakayoona katika wilaya ya Babeli, pamoja na vitu watakavyotoa watu kwa hiari yao, na vitu vya makuhani walivyotoa kwa hiari yao, kwa ajili ya nyumba ya Mungu wao iliyoko Yerusalemu. 17 Kwa sababu hiyo ujitahidi kununua kwa fedha hiyo mafahali, kondoo waume, wana-kondoo, pamoja na sadaka zao za unga, na sadaka zao za kinywaji; nawe utazitoa juu ya madhabahu ya nyumba ya Mungu wenu, iliyoko Yerusalemu. 18 Na neno lo lote mtakaloona vema kulitenda, wewe na ndugu zako, kwa ile fedha na dhahabu itakayobaki, hilo litendeni, kama apendavyo Mungu wenu. 19 Na vile vyombo upewavyo kwa huduma ya nyumba ya Mungu wako, virejeze mbele za Mungu wa Yerusalemu. 20 Na cho chote kitakachohitajiwa zaidi, kwa ajili ya nyumba ya Mungu wako, kitakachokupasa kukitoa, kitoe katika nyumba ya hazina ya mfalme. 21 Na mimi, naam mimi, mfalme Artashasta, nawapa amri wote wenye kutunza hazina, walio ng'ambo ya Mto, ya kwamba, kila neno ambalo Ezra, kuhani, mwandishi wa torati ya Mungu wa mbinguni, atalitaka kwenu, na litendeke kwa bidii nyingi, 22 hata kiasi cha talanta mia za fedha, na vipimo mia vya ngano, na bathi mia za divai, na bathi mia za mafuta, na chumvi bila kuuliza kiasi chake. 23 Kila neno litakaloamriwa na Mungu wa mbinguni, na litendeke halisi kwa ajili ya nyumba ya Mungu wa mbinguni. Kwa nini itokee ghadhabu juu ya ufalme wa mfalme na wanawe? 24 Tena twawaarifuni ya kuwa katika habari ya makuhani, na Walawi, na waimbaji, na mabawabu na Wanethini, au watumishi wa nyumba hii ya Mungu, si halali kuwatoza kodi, wala ada, wala ushuru. 25 Na wewe, Ezra, kwa kadiri ya hekima ya Mungu wako iliyo mkononi mwako, waweke waamuzi na makadhi, watakaowahukumu watu wote walio ng'ambo ya Mto, yaani, wote wenye kuzijua amri za Mungu wako; ukamfundishe yeye asiyezijua. 26 Na kila mtu asiyekubali kuitenda sheria ya Mungu wako, na sheria ya mfalme, na apatilizwe hukumu kwa bidii, kwamba ni kuuawa, au kwamba ni kuhamishwa, au kuondolewa mali yake, au kufungwa. 27 Na ahimidiwe Bwana, Mungu wa baba zetu, aliyetia neno kama hilo katika moyo wa mfalme, kuipamba nyumba ya Bwana iliyoko Yerusalemu. 28 Naye amenifikilizia rehema zake mbele ya mfalme, na washauri wake, na mbele ya wakuu wote wa mfalme wenye mamlaka. Nami nikatiwa nguvu, kwa kadiri mkono wa Bwana, Mungu wangu, ulivyokuwa pamoja nami, nikawakusanya wakuu wote katika Israeli, ili wakwee pamoja nami.

Ezra 8

1 Basi hawa ndio wakuu wa mbari za baba zao, na hii ndiyo nasaba ya wale waliokwea pamoja nami kutoka Babeli, wakati wa kutawala kwake mfalme Artashasta. 2 Wa wana wa Finehasi, Gershoni; wa wana wa Ithamari, Danieli; wa wana wa Daudi, Hatushi, mwana wa Shekania; 3 wa wana wa Paroshi, Zekaria; na pamoja naye wakahesabiwa kwa nasaba wanaume mia na hamsini. 4 Wa wana wa Pahath-Moabu, Eliehoenai, mwana wa Zerahia; na pamoja naye wanaume mia mbili; 5 Wa wana wa Zatu, Shekania, mwana wa Yahazieli; na pamoja naye wanaume mia tatu. 6 Na wa wana wa Adini, Ebedi, mwana wa Yonathani; na pamoja naye wanaume hamsini. 7 Na wa wana wa Elamu, Yeshaya, mwana wa Athalia; na pamoja naye wanaume sabini. 8 Na wa wana wa Shefatia, Zebadia, mwana wa Mikaeli; na pamoja naye wanaume themanini. 9 Wa wana wa Yoabu, Obadia, mwana wa Yehieli; na pamoja naye wanaume mia mbili na kumi na wanane. 10 Na wa wana wa Binui, Shelomithi, mwana wa Yosifia; na pamoja naye wanaume mia na sitini. 11 Na wa wana wa Bebai, Zekaria, mwana wa Bebai; na pamoja naye wanaume ishirini na wanane. 12 Na wa wana wa Azgadi, Yohana, mwana wa Hakatani; na pamoja naye wanaume mia na kumi. 13 Na wa wana wa Adonikamu, hawa waliokuwa wa mwisho, na hayo ndiyo majina yao, Elifeleti, na Yeueli, na Shemaya; na pamoja nao wanaume sitini. 14 Na wa wana wa Bigwai, Uthai, mwana wa Zabudi; na pamoja naye wanaume sabini. 15 Nikawakusanya penye mto ushukao kwenda Ahava; na huko tukapiga kambi yetu muda wa siku tatu; nikawakagua watu, na makuhani, wala sikuona hapo wana wa Lawi hata mmoja. 16 Ndipo nikatuma watu kwenda kumwita Eliezeri, na Arieli, na Shemaya, na Elnathani, na Yaribu, na Elnathani, na Nathani, na Zekaria, na Meshulamu, waliokuwa wakuu; na Yoyaribu, na Elnathani pia, waliokuwa waalimu. 17 Nikawapeleka kwa Ido, mkuu, huko Kasifia; nikawaambia watakayomwambia Ido, na ndugu zake hao Wanethini, huko Kasifia, kwamba watuletee watu watakaohudumu katika nyumba ya Mungu wetu. 18 Na kama mkono mwema wa Mungu wetu ulivyokuwa pamoja nasi, wakamletea Ishekeli, mmoja wa wana wa Mali ,mwana wa Lawi, mwana wa Israeli;na Sherebia ,pamoja na wanawe na ndugu zake ,watu kumi na wanawe. 19 na Hashabia, na pamoja naye Yeshaya, wa wana wa Merari, na ndugu zake na wana wao, watu ishirini; 20 na katika Wanethini, ambao Daudi, na wakuu, walikuwa wamewaweka kwa ajili ya utumishi wa Walawi, Wanethini mia mbili na ishirini; wote wametajwa kwa majina yao. 21 Ndipo nikaamuru kufunga, hapo penye mto Ahava, ili tupate kujinyenyekeza mbele za Mungu, na kutafuta kwake njia iliyonyoka, kwa ajili yetu sisi wenyewe, na kwa ajili ya watoto wetu, na kwa mali yetu yote. 22 Maana naliona haya kumwomba mfalme kikosi cha askari na wapanda farasi, ili kutusaidia juu ya adui njiani; kwa maana tulikuwa tumesema na mfalme, tukinena, Mkono wa Mungu u juu ya watu wote wamtafutao, kuwatendea mema; bali uweza wake na ghadhabu yake ni kinyume cha wote wamwachao. 23 Basi tukafunga, tukamsihi Mungu wetu kwa ajili ya hayo; naye akatutakabali. 24 Ndipo nikawatenga watu kumi na wawili wa wakuu wa makuhani, nao ni Sherebia, na Hashabia, na watu kumi wa ndugu zao pamoja nao, 25 nami nikawapimia kwa mizani zile fedha, na dhahabu, na vile vyombo, matoleo kwa ajili ya nyumba ya Mungu wetu, ambayo mfalme, na washauri wake, na wakuu wake, na Israeli wote waliokuwapo, walikuwa wameyatoa; 26 nami nikawapimia mikononi mwao talanta za fedha mia sita na hamsini na vyombo vya fedha talanta mia; na talanta mia za dhahabu; 27 na mabakuli ishirini ya dhahabu, thamani yake darkoni elfu; na vyombo viwili vya shaba nzuri iliyong'aa, thamani yake sawa na dhahabu. 28 Kisha nikawaambia, Ninyi mmekuwa watakatifu kwa Bwana, na hivyo vyombo ni vitakatifu; na fedha na dhahabu ni matoleo ya hiari kwa Bwana, Mungu wa baba zenu. 29 Basi, angalieni, na kuvitunza vitu hivi, hata mtakapovipima mbele ya wakuu wa makuhani, na Walawi, na wakuu wa mbari za mababa wa Israeli, huko Yerusalemu, katika vyumba vya nyumba ya Bwana. 30 Hivyo makuhani na Walawi wakaupokea uzani wa fedha, na dhahabu, na vyombo, ili kuvileta Yerusalemu nyumbani kwa Mungu wetu. 31 Ndipo tukasafiri toka mtoni Ahava siku ya kumi na mbili ya mwezi wa kwanza, ili kwenda Yerusalemu; na mkono wa Mungu ulikuwa pamoja nasi, akatuokoa na mkono wa adui, na mtu mwenye kutuvizia njiani. 32 Tukafika Yerusalemu, tukakaa huko muda wa siku tatu. 33 Hata siku ya nne, hizo fedha na dhahabu na vile vyombo vilipimwa ndani ya nyumba ya Mungu, vikatiwa mikononi mwa Meremothi, mwana wa Uria, kuhani; na pamoja naye alikuwapo Eleazari, mwana wa Finehasi; na pamoja nao Yozabadi, mwana wa Yeshua, na Noadia, mwana wa Binui, Walawi; 34 vile vyombo vyote kwa hesabu na kwa uzani; tena uzani wake wote uliandikwa wakati ule. 35 Na wana wa uhamisho, waliokuwa wametoka katika uhamisho wakamtolea Mungu wa Israeli sadaka za kuteketezwa, ng'ombe kumi na wawili kwa ajili ya Israeli wote, na kondoo waume tisini na sita, na wana-kondoo sabini na saba, na mbuzi waume kumi na wawili, kuwa sadaka ya dhambi, hao wote pia walikuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana. 36 Wakawapa manaibu wa mfalme, na maliwali wa ng'ambo ya Mto, maagizo ya mfalme; nao wakawapa watu, na nyumba ya Mungu, msaada.

Ezra 9

1 Na mambo hayo yalipokwisha kutendeka, wakuu wakanikaribia, wakisema, Watu wa Israeli, na makuhani, na Walawi, hawakujitenga na watu wa nchi hizi, wamefanya sawasawa na machukizo yao, yaani, ya Wakanaani, na Wahiti, na Waperizi, na Wayebusi, na Waamoni, na Wamoabi, na Wamisri, na Waamori. 2 Maana wametwaa binti zao kuwa wake zao, na wake za watoto wao; basi mbegu takatifu wamejichanganya na watu wa nchi hizi; naam, mkono wa wakuu na mashehe umetangulia katika kosa hili. 3 Nami niliposikia hayo, nikararua nguo yangu na joho yangu, nikang'oa nywele za kichwa changu, na ndevu zangu, nikaketi kwa mshangao. 4 Ndipo wakanikusanyikia watu wote walioyatetemekea maneno ya Mungu wa Israeli, kwa sababu ya lile kosa la watu wa uhamisho; nami nikaketi kwa mshangao hata wakati wa sadaka ya jioni. 5 Na wakati wa sadaka ya jioni nikainuka baada ya kunyenyekea kwangu, nguo yangu na joho yangu zimeraruliwa, nikaanguka magotini nikakunjua mikono yangu mbele za Bwana, Mungu wangu; 6 nikasema, Ee Mungu wangu, nimetahayari, naona haya kuinua uso wangu mbele zako, Mungu wangu; kwa maana maovu yetu ni mengi, hata yamefika juu ya vichwa vyetu, na hatia yetu imeongezeka na kufika mbinguni. 7 Tangu siku za baba zetu tumekuwa na hatia kupita kiasi hata leo; na kwa sababu ya maovu yetu sisi, na wafalme wetu, na makuhani wetu, tumetiwa katika mikono ya wafalme wa nchi hizi, tumepigwa kwa upanga, tumechukuliwa mateka, tumenyang'anywa mali zetu, tumetiwa haya nyuso zetu, kama hivi leo. 8 Na sasa kwa muda kidogo tumeneemeshwa na Bwana, Mungu wetu, hata akatuachia mabaki yaokoke, akatupa msumari katika mahali pake patakatifu. Mungu wetu atutie nuru machoni mwetu, tuburudike kidogo katika kufungwa kwetu. 9 Maana sisi tu watumwa; lakini Mungu wetu hakutuacha katika utumwa wetu, bali ametufikilizia rehema zake, mbele ya wafalme wa Uajemi, ili kutuburudisha, kuisimamisha nyumba ya Mungu wetu, na kuitengeneza palipobomoka, atupe ukuta katika Yuda na Yerusalemu. 10 Na sasa, Ee Mungu wetu, tuseme nini baada ya hayo? Maana tumeziacha amri zako, 11 ulizoziamuru kwa midomo ya watumishi wako, manabii, ukisema, Nchi ile, mnayoiendea ili kuimiliki, ni nchi ya uchafu, kwa sababu ya uchafu wa watu wa nchi zile, kwa ajili ya machukizo yao, yaliyoijaza tangu upande huu mpaka upande huu, kwa uchafu wao. 12 Basi, msiwape wana wao binti zenu, wala msitwae binti zao kuwa wake za wana wenu, wala msiwatakie amani wala kufanikiwa milele; ili mpate kuwa hodari, na kula wema wa nchi hiyo, na kuwaachia watoto wenu iwe urithi wa milele. 13 Na baada ya hayo yote yaliyotupata kwa sababu ya matendo yetu mabaya, na kwa sababu ya hatia yetu iliyo kuu, ikiwa wewe Mungu wetu hukutuadhibu kama tulivyostahili kwa maovu yetu, tena umetupa mabaki; 14 je! Tuzivunje tena amri zako, tukajiunge na watu wanaotenda machukizo hayo, kwa kuoana nao? Je! Usingekasirika nasi hata kutuangamiza kabisa, pasisalie mabaki yo yote, wala mtu wa kuokoka? 15 Ee Bwana, Mungu wa Israeli, wewe ndiwe mwenye haki, maana sisi tumesalia, mabaki yaliyookoka, kama hivi leo; tazama, sisi tupo hapa wenye hatia mbele zako; maana hapana mtu awezaye kusimama mbele zako kwa sababu ya jambo hili.

Ezra 10

1 Basi hapo Ezra alipokuwa akiomba na kuungama, akilia, na kujiangusha kifudifudi mbele ya nyumba ya Mungu, wakamkusanyikia katika Israeli wote kusanyiko kubwa sana la wanaume, na wanawake, na watoto; maana watu hao walikuwa wakilia sana. 2 Hata Shekania, mwana wa Yehieli, mmoja wa wana wa Elamu, akajibu, akamwambia Ezra, Sisi tumemkosa Mungu wetu, nasi tumeoa wanawake wageni wa watu wa nchi hizi; lakini kungaliko tumaini kwa Israeli katika jambo hili. 3 Haya basi! Na tufanye agano na Mungu wetu, kuachana na wake zetu, na wale waliozaliwa nao, tukilifuata shauri la bwana wangu, na shauri la hao wanaoitetemekea amri ya Mungu wetu; mambo haya na yatendeke kwa kuifuata torati. 4 Inuka; maana shughuli hii yakuhusu wewe; na sisi tu pamoja nawe; uwe na moyo mkuu, ukaitende. 5 Ndipo Ezra akaondoka, akawaapisha wakuu wa makuhani, na Walawi, na Israeli wote, ya kwamba watafanya kama hayo. Basi wakaapa. 6 Kisha Ezra akaondoka hapo mbele ya nyumba ya Mungu, akaingia katika chumba cha Yehohanani, mwana wa Eliashibu; hata, alipofika huko, hakula mkate, wala hakunywa maji; kwa maana alilia kwa sababu ya kosa lile la watu wa uhamisho. 7 Wakapiga mbiu katika Yuda yote na Yerusalemu, ya kwamba wana wote wa uhamisho wakusanyike pamoja huko Yerusalemu; 8 na ya kwamba mtu awaye yote asiyekuja katika muda wa siku tatu, kwa shauri lile la wakuu na wazee, basi aondolewe mali zake zote, akatengwe yeye mwenyewe na mkutano wa uhamisho. 9 Ndipo wanaume wote wa Yuda na Benyamini wakakusanyika katika muda wa siku tatu; ulikuwa mwezi wa kenda, siku ya ishirini ya mwezi; na watu wote wakaketi katika uwanja mbele ya nyumba ya Mungu, wakitetemeka kwa sababu ya neno hilo, na kwa sababu ya mvua kubwa. 10 Kisha Ezra, kuhani, akasimama, akawaambia, Mmekosa, mmeoa wanawake wageni, kuiongeza hatia ya Israeli. 11 Sasa basi, ungameni mbele za Bwana, Mungu wa baba zenu, mkatende alipendalo; mkajitenge na watu wa nchi, tena na wanawake wageni. 12 Ndipo mkutano wote wakajibu, wakasema, kwa sauti kuu, Kama ulivyosema katika habari yetu, ndivyo vitupasavyo kutenda. 13 Lakini watu hawa ni wengi, tena ni wakati wa mvua nyingi, nasi hatuwezi kusimama nje, tena kazi hii si kazi ya siku moja, wala ya siku mbili; maana tumekosa sana katika jambo hili. 14 Basi maakida wetu na wawekwe kwa ajili ya mkutano wote, na watu wote walio katika miji yetu, waliooa wanawake wageni, na waje nyakati zilizoamriwa, tena pamoja nao na waje wazee wa kila mji, na makadhi wa miji hiyo, hata ghadhabu kali ya Mungu wetu itakapotuondokea mbali, jambo hili likamalizike. 15 Yonathani, mwana wa Asaheli, na Yazeya, mwana wa Tikwa, hawa peke yao ndio waliosimama kulipinga neno hilo; na Meshulamu, na Shabethai Mlawi, wakawasaidia. 16 Basi wana wa uhamisho wakafanya hivyo. Na Ezra, kuhani, akatengwa, pamoja na baadhi ya wakuu wa mbari za mababa, kwa hesabu ya mbari ya baba zao; na hao wote kwa majina yao. Wakaketi siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, ili kulichunguza jambo hilo. 17 Wakamaliza mambo ya wanaume wote, waliokuwa wameoa wanawake wageni, siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza. 18 Basi, miongoni mwa makuhani walionekana wengine waliokuwa wameoa wanawake wageni; wa wana wa Yoshua, mwana wa Yosadaki, na nduguze; Maaseya, na Eliezeri, na Yaribu, na Gedalia. 19 Nao wakatoa ahadi ya kwamba wataachana na wake zao; na kwa kuwa walikuwa na hatia, wakatoa kondoo mume kwa hatia yao. 20 Na wa wana wa Imeri; Hanani, na Zebadia. 21 Na wa wana wa Harimu; Maaseya, na Eliya, na Shemaya, na Yehieli, na Uzia. 22 Na wa wana wa Pashuri; Elioenai, na Maaseya, na Ishmaeli, na Nethaneli, na Yozabadi, na Elasa. 23 Na wa Walawi; Yozabadi, na Shimei, na Kelaya (ndiye Kelita), na Pethahia, na Yuda, na Eliezeri. 24 Na wa waimbaji; Eliashibu. Na wa mabawabu; Shalumu, na Telemu, na Uri. 25 Na wa Israeli; wa wana wa Paroshi; Ramia, na Izia, na Malkiya, na Miyamini, na Eleazari, na Malkiya, na Benaya. 26 Na wa wana wa Elamu; Matania, na Zekaria, na Yehieli, na Abdi, na Yeremothi, na Eliya. 27 Na wa wana wa Zatu; Elioenai, na Eliashibu, na Matania, na Yeremothi, na Zabadi, na Aziza. 28 Na wa wana wa Bebai; Yehohanani, na Hanania, na Zakai, na Athlai. 29 Na wa wana wa Bani; Meshulamu, na Maluki, na Adaya, na Yashubu, na Sheali, na Yeremothi. 30 Na wa wana wa Pahath-Moabu; Adna, na Kelali, na Benaya, na Maaseya, na Matania, na Besaleli, na Binui, na Manase. 31 Na wa wana wa Harimu; Eliezeri, na Ishiya, na Malkiya, na Shemaya, na Shimeoni, 32 na Benyamini, na Maluki, na Shemaria. 33 Na wa wana wa Hashumu; Matenai, na Matata, na Zabadi, na Elifeleti, na Yeremai, na Manase, na Shimei. 34 Na wa wana wa Bani; Maadai, na Amramu, na Ueli, 35 na Benaya, na Bedeya, na Keluhi, 36 na Wania, na Meremothi, na Eliashibu, 37 na Matania, na Matenai, na Yaasu. 38 Na wa wana wa Binui; Shimei, 39 na Shelemia, na Nathani, na Adaya, 40 na Maknadebai, na Shashai, na Sharai, 41 na Azareli, na Shelemia, na Shemaria, 42 na Shalumu, na Amaria, na Yusufu. 43 Na wa wana wa Nebo; Yeieli, na Matithia, na Zabadi, na Zebina, na Ido, na Yoeli, na Benaya. 44 Hao wote walikuwa wameoa wanawake wageni; na wake zao wengine walikuwa wamezaa watoto.

Nehemia 1

1 Habari za Nehemia, mwana wa Hakalia. Ikawa katika mwezi wa Kisleu, mwaka wa ishirini, nilipokuwapo Shushani ngomeni, 2 Hanani, mmoja wa ndugu zangu, akanijia, yeye na watu wengine waliotoka Yuda; nami nikawauliza habari za Wayahudi waliopona, hao watu wa uhamisho waliosalia; na habari za Yerusalemu. 3 Wakaniambia, Watu wa uhamisho, waliosalia huko katika wilaya ile, wamo katika hali ya dhiki nyingi na mashutumu; tena ukuta wa Yerusalemu umebomolewa, na malango yake yameteketezwa kwa moto. 4 Hata ikawa niliposikia maneno hayo, nikaketi, nikalia, nikaomboleza siku kadha wa kadha; kisha nikafunga, nikaomba mbele za Mungu wa mbinguni; 5 nikasema, Nakusihi, Ee Bwana, Mungu wa mbinguni, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, mwenye kutimiza agano lake na rehema zake kwa hao wampendao na kuzishika amri zake; 6 tega sikio lako, macho yako yakafumbuke, upate kuyasikiliza maombi ya mtumishi wako, ninayoomba mbele zako wakati huu, mchana na usiku, kwa ajili ya wana wa Israeli, watumishi wako; hapo ninapoziungama dhambi za wana wa Israeli, tulizozifanya juu yako; naam, mimi na nyumba ya baba yangu tumefanya dhambi. 7 Tumetenda maovu mengi juu yako, wala hatukuzishika amri, wala sheria, wala hukumu, ulizomwamuru Musa, mtumishi wako. 8 Nakuomba, likumbuke neno lile ulilomwamuru Musa, mtumishi wako, ukisema, Mkikosa, nitawatawanya kati ya mataifa; 9 bali mkinirudia mimi, na kuzishika amri zangu na kuzitenda, watu wako waliofukuzwa wajapokuwa katika pande za mwisho za mbingu, hata hivyo nitawakusanya kutoka huko, na kuwaleta mpaka mahali pale nilipopachagua ili kuliweka jina langu hapo. 10 Basi watu hao ni watumishi wako na watu wako, uliowakomboa kwa uweza wako mwingi, na kwa mkono wako hodari. 11 Ee Bwana, nakusihi, litege sikio lako, uyasikilize maombi ya mtumishi wako, na maombi ya watumishi wako, wanaofurahi kulicha jina lako; nakuomba sana; unifanikishe mimi, mtumishi wako, leo, ukanijalie rehema mbele ya mtu huyu. (Maana, nalikuwa mnyweshaji wa mfalme).

Nehemia 2

1 Ikawa katika mwezi wa Nisani, mwaka wa ishirini wa mfalme Artashasta, na divai imewekwa mbele yake, nikaishika ile divai, nikampa mfalme. Nami mpaka sasa sikuwa na huzuni mbele ya mfalme wakati wo wote. 2 Basi mfalme akaniambia, Mbona umesikitika uso wako, nawe huna ugonjwa? Nini hii, isipokuwa ni huzuni ya moyo? Ndipo nikaogopa sana. 3 Nikamwambia mfalme, Mfalme na aishi milele; kwani uso wangu usiwe na huzuni, iwapo mji, ulio mahali pa makaburi ya baba zangu, unakaa ukiwa, na malango yake yameteketezwa kwa moto? 4 Ndipo mfalme akaniambia, Una haja gani unayotaka kuniomba? Basi nikamwomba Mungu wa mbinguni. 5 Nikamwambia mfalme, Mfalme akiona vema, na ikiwa mimi, mtumishi wako, nimepata kibali machoni pako, tafadhali unipeleke mpaka Yuda, niuendee mji wa makaburi ya baba zangu, nipate kuujenga. 6 Mfalme akaniuliza, (malkia naye ameketi karibu naye), Safari yako itakuwa ya siku ngapi? Nawe utarudi lini? Hivyo mfalme akaona vema kunipeleka; nami nikampa muda. 7 Tena nikamwambia mfalme, Mfalme akiona vema, na nipewe nyaraka kwa maliwali walio ng'ambo ya Mto, ili waniache kupita mpaka nifike Yuda; 8 nipewe na waraka kwa Asafu, mwenye kuutunza mwitu wa mfalme, ili anipe miti ya kufanyizia boriti kwa malango ya ngome ya nyumba, na kwa ukuta wa mji; na kwa nyumba ile nitakayoingia mimi. Naye mfalme akanipa, kama mkono mwema wa Mungu wangu ulivyokuwa juu yangu. 9 Ndipo nikafika kwa maliwali walio ng'ambo ya Mto, nikawapa hizo nyaraka za mfalme. Naye mfalme alikuwa amepeleka maakida wa jeshi lake na wapanda farasi pamoja nami. 10 Hata Sanbalati, Mhoroni, na Tobia, mtumishi wake, Mwamoni, waliposikia habari hizi, ziliwahuzunisha sana, kwa kuwa amekuja mtu kuwatakia heri wana wa Israeli. 11 Basi nikafika Yerusalemu, nikakaa huko muda wa siku tatu. 12 Kisha nikaondoka usiku, mimi na watu wachache pamoja nami; wala sikumwambia mtu neno hili alilolitia Mungu wangu moyoni mwangu, nilitende kwa ajili ya Yerusalemu; wala hapakuwa na mnyama pamoja nami, ila mnyama yule niliyempanda mwenyewe. 13 Nikatoka nje usiku, kwa njia ya lango la bondeni, nikashika njia iendayo kisima cha joka, na lango la jaa; nikazitazama kuta za Yerusalemu, zilizokuwa zimebomoka; na malango yake yameteketezwa kwa moto. 14 Kisha nikaendelea mpaka lango la chemchemi, na ziwa la mfalme; lakini hapakuwa na nafasi ya kupita kwa yule mnyama aliyekuwa chini yangu. 15 Kisha nikapanda usiku kando ya kijito, nikautazama ukuta; kisha nikarudi nyuma, nikaingia kwa lango la bondeni, nikarejea hivyo. 16 Wala mashehe hawakujua nilikokwenda, wala nilivyotenda; wala sijawaambia Wayahudi, wala makuhani, wala wakuu, wala mashehe, wala watu wengine waliokuwa wakiifanya kazi hiyo. 17 Kisha nikawaambia, Mnaona hali hii dhaifu tuliyo nayo, jinsi Yerusalemu ulivyo hali ya ukiwa, na malango yake yalivyoteketezwa kwa moto; haya! Na tuujenge tena ukuta wa Yerusalemu, ili tusiwe shutumu tena. 18 Nikawaeleza habari ya mkono wa Mungu wangu ulivyokuwa mwema juu yangu; pia na maneno ya mfalme aliyoniambia. Nao wakasema, Haya! Na tuondoke tukajenge. Basi wakaitia mikono yao nguvu kwa kazi hiyo njema. 19 Lakini waliposikia Sanbalati, Mhoroni, na Tobia, mtumishi wake, Mwamoni, na Geshemu, Mwarabu, walitucheka, wakatudharau, wakasema, Ni nini neno hili mnalofanya? Je! Mtaasi ninyi juu ya mfalme? 20 Ndipo nikawajibu, nikawaambia, Mungu wa mbinguni, yeye atatufanikisha; kwa hiyo sisi, watumishi wake, tutaondoka na kujenga; lakini ninyi hamna sehemu, wala haki, wala kumbukumbu, katika Yerusalemu.

Nehemia 3

1 Ndipo akaondoka Eliashibu, kuhani mkuu, pamoja na nduguze makuhani, wakalijenga lango la kondoo; wakazitia boriti zake, wakaisimamisha milango yake; mpaka mnara wa Hamea wakalitakasa, mpaka mnara wa Hananeli. 2 Na baada yao wakajenga watu wa Yeriko. Na baada yao akajenga Zakuri, mwana wa Imri. 3 Na lango la samaki wakalijenga wana wa Senaa; wakazitia boriti zake, wakaisimamisha milango yake, na vyuma vyake, na makomeo yake. 4 Na baada yao akafanyiza Meremothi, mwana wa Uria, mwana wa Hakosi. Na baada yao akafanyiza Meshulamu, mwana wa Berekia, mwana wa Meshezabeli. Na baada yao akafanyiza Sadoki, mwana wa Baana. 5 Na baada yao wakafanyiza Watekoi; lakini wakuu wao hawakutia shingo zao kazini mwa bwana wao. 6 Na lango la kale wakalifanyiza Yoyada, mwana wa Pasea, na Meshulamu, mwana wa Besodeya; wakazitia boriti zake, wakaisimamisha milango yake, na vyuma vyake, na makomeo yake. 7 Na baada yao wakafanyiza Melatia, Mgibeoni, na Yadoni, Mmeronothi, watu wa Gibeoni, na wa Mispa, raia wa kiti cha enzi cha liwali wa ng'ambo ya Mto. 8 Na baada yao akafanyiza Uzieli, mwana wa Harhaya, mmoja wa mafundi wa dhahabu. Na baada yake akafanyiza Hanania, mmoja wa mafundi wa manukato, nao wakaujengea Yerusalemu buruji mpaka ule ukuta mpana. 9 Na baada yao akafanyiza Refaya, mwana wa Huri, akida wa nusu ya Yerusalemu. 10 Na baada yao akafanyiza Yedaya, mwana wa Harumafu, kuielekea nyumba yake. Na baada yake akafanyiza Hatushi, mwana wa Hashabneya. 11 Malkiya, mwana wa Harimu, na Hashubu, mwana wa Pahath-moabu, wakafanyiza sehemu nyingine, na mnara wa tanuu. 12 Na baada yake akafanyiza Shalumu, mwana wa Haloheshi, akida wa nusu ya Yerusalemu, yeye na binti zake. 13 Lango la bondeni wakalifanyiza Hanuni, nao wakaao Zanoa; wakalijenga, wakaisimamisha milango yake, na vyuma vyake, na makomeo yake, na huo ukuta wa dhiraa elfu mpaka lango la jaa. 14 Na lango la jaa akalifanyiza Malkiya, mwana wa Rekabu, akida wa mtaa wa Beth-hakeremu; akalijenga, akaisimamisha milango yake, na vyuma vyake, na makomeo yake. 15 Na lango la chemchemi akalifanyiza Shalumu, mwana wa Kolhoze, akida wa mtaa wa Mispa; akalijenga na kulifunika, akaisimamisha milango yake, na vyuma vyake, na makomeo yake, na huo ukuu wa birika la Shiloa karibu na bustani ya mfalme, mpaka madaraja yashukayo kutoka mji wa Daudi. 16 Baada yake akafanyiza Nehemia, mwana wa Azbuki, akida wa nusu ya mtaa wa Beth-suri, mpaka mahali paelekeapo makaburi ya Daudi, na mpaka birika lililofanyizwa, na mpaka nyumba ya mashujaa. 17 Baada yake wakafanyiza Walawi, Rehumi, mwana wa Bani. Baada yake akafanyiza Hashabia, akida wa nusu ya mtaa wa Keila, kwa mtaa wake. 18 Baada yake wakafanyiza ndugu zao, Binui, mwana wa Henadadi, akida wa nusu ya mtaa wa Keila. 19 Na baada yake akafanyiza Ezeri, mwana wa Yeshua, akida wa Mispa, sehemu nyingine, kupaelekea penye kupanda kwa ghala ya silaha, ukuta ugeukapo. 20 Baada yake Baruki, mwana wa Zakai, akafanyiza kwa bidii sehemu nyingine, toka ugeukapo ukuta mpaka mlango wa nyumba ya Eliashibu, kuhani mkuu. 21 Baada yake akafanyiza Meremothi, mwana wa Uria, mwana wa Hakosi, sehemu nyingine, toka mlango wa nyumba ya Eliashibu mpaka mwisho wa nyumba ya Eliashibu. 22 Na baada yake wakafanyiza makuhani, watu wa Uwandani. 23 Baada yao wakafanyiza Benyamini na Hashubu, kuielekea nyumba yao. Baada yao akafanyiza Azaria, mwana wa Maaseya, mwana wa Anania, kando ya nyumba yake. 24 Baada yake akafanyiza Binui, mwana wa Henadadi, sehemu nyingine, toka nyumba ya Azaria mpaka ugeukapo ukuu, na mpaka pembeni. 25 Baada yake akafanyiza Palali, mwana wa Uzai, kuelekea ugeukapo ukuta, nao mnara utokezao penye nyumba ya juu ya kifalme, iliyopo karibu na uwanda wa walinzi. Baada yake akafanyiza Pedaya, mwana wa Paroshi, 26 (basi Wanethini hukaa Ofeli), mpaka mahali paelekeapo lango la maji kukabili mashariki, nao mnara utokezao. 27 Baada yake wakafanyiza Watekoi sehemu nyingine, kuuelekea mnara mkubwa utokezao, na mpaka ukuta wa Ofeli. 28 Juu ya lango la farasi wakafanyiza makuhani, kila mtu kuielekea nyumba yake. Baada yao akafanyiza Sadoki, mwana wa Imeri, kuielekea nyumba yake. 29 Na baada yake akafanyiza Shemaya, mwana wa Shekania, mlinzi wa lango la mashariki. 30 Baada yake wakafanyiza Hanania, mwana wa Shelemia, na Hanuni, mwana wa sita wa Salafu, sehemu nyingine. Baada yake akafanyiza Meshulamu, mwana wa Berekia, sehemu nyingine kuelekea chumba chake. 31 Baada yake akafanyiza Malkiya, mmoja wa mafundi wa dhahabu, mpaka nyumba ya Wanethini, na ya wafanya biashara, kulielekea lango la gereza, na mpaka chumba cha juu cha pembeni. 32 Na kati ya chumba cha juu cha pembeni na lango la kondoo wakafanyiza mafundi wa dhahabu na wafanya biashara.

Nehemia 4

1 Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. 2 Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? 3 Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe. 4 Sikia, Ee Mungu wetu; maana tunadharauliwa; ukawarudishie mashutumu yao juu ya vichwa vyao, ukawatoe watekwe katika nchi ya uhamisho; 5 wala usiusitiri uovu wao, wala isifutwe dhambi yao, mbele zako; kwa maana wamekukasirisha mbele ya hao wanaojenga. 6 Basi tukaujenga ukuta; nao ukuta wote ukaungamanishwa kiasi cha nusu ya kimo chake; maana watu walikuwa na moyo wa kufanya kazi. 7 Lakini ikawa, Sanbalati, na Tobia, na Waarabu, na Waamoni, na Waashdodi, waliposikia ya kuwa kazi ya kuzitengeneza kuta za Yerusalemu inaendelea, na ya kuwa mahali palipobomoka panaanza kuzibwa, basi wakaghadhibika mno; 8 wakafanya shauri wote pamoja kuja kupigana na Yerusalemu, na kufanya machafuko humo. 9 Bali sisi tulimwomba dua Mungu wetu, tena tukaweka walinzi, mchana na usiku, kwa sababu yao, ili kuwapinga. 10 Wakasema Yuda, Nguvu zao wachukuao mizigo zimedhoofika, na kifusi tele zipo; tusiweze kuujenga ukuta. 11 Nao adui zetu wakasema, Hawatajua wala kuona, hata tutakapokuja kati yao, na kuwaua, na kuikomesha kazi hiyo. 12 Kisha ikawa, Wayahudi walipokuja, wale waliokaa karibu nao, wakatuambia mara kumi, Kutoka kila mahali mtakaporejea watatushambulia. 13 Basi, nikaweka watu, mahali pa chini pa nafasi iliyokuwa nyuma ya ukuta, mahali palipokuwa wazi, kwa kadiri ya jamaa zao, nikawaweka wenye panga zao, na mikuki yao, na pinde zao. 14 Nikatazama, nikaondoka, nikawaambia wakuu, na mashehe, na watu wengine waliobaki, Msiwaogope; mkumbukeni Bwana, aliye mkuu mwenye kuogofya, mkawapiganie ndugu zenu, na wana wenu, na binti zenu, na wake zenu, na nyumba zenu. 15 Kisha ikawa, adui zetu waliposikia ya kuwa tumekwisha kupata habari, na ya kuwa Mungu amelibatilisha shauri lao, ndipo sisi sote tukarudi ukutani, kila mtu kwa kazi yake. 16 Ikawa tokea wakati huo, nusu ya watumishi wangu walitumika katika kazi hiyo, na nusu yao wakaishika mikuki, na ngao, na pinde, na darii; na maakida walikuwa nyuma ya nyumba yote ya Yuda. 17 Watu wale walioujenga ukuta, na wale waliochukua mizigo, walijitweka wenyewe, kila mtu alifanya kazi kwa mkono mmoja, na kwa mkono wake wa pili alishika silaha yake; 18 nao wajenzi, kila mtu alikuwa na upanga wake, umefungwa ubavuni mwake, ndivyo alivyojenga. Na yeye aliyepiga baragumu alikuwa karibu na mimi. 19 Nikawaambia wakuu, na mashehe na watu wengine; Kazi hii ni nyingi, tena kubwa, nasi tumetawanyika juu ya ukuta, kila mtu mbali na mwenzake; 20 basi mahali po pote mtakaposikia sauti ya baragumu, enendeni huko, mkatujie; Mungu wetu atatupigania. 21 Hivyo tukajitia katika kazi hiyo; na nusu yao waliishika mikuki, tangu alfajiri hata nyota zikatokea. 22 Kadhalika, wakati ule ule, nikawaambia watu, Kila mtu na akae ndani ya Yerusalemu pamoja na mtumishi wake, wapate kuwa walinzi wetu wakati wa usiku, na kufanya kazi wakati wa mchana. 23 Basi mimi, na ndugu zangu, na watumishi wangu, na watu wa ulinzi walionifuata, hatukuvua nguo zetu hata mmoja; kila mtu alikwenda kuteka maji akichukua silaha yake.

Nehemia 5

1 Ndipo kukatokea kilio kikuu cha watu, na wake zao, juu ya ndugu zao Wayahudi. 2 Maana, walikuwako watu waliosema, Sisi, na wana wetu na binti zetu, tu wengi; na tupate ngano, tule, tukaishi. 3 Tena walikuwako wengine waliosema, Tumeweka rehani mashamba yetu, na mizabibu yetu, na nyumba zetu; tupate ngano, kwa sababu ya njaa. 4 Tena walikuwako wengine waliosema, Tumekopa fedha ili kulipa kodi ya mfalme kwa kuweka rehani mashamba yetu, na mizabibu yetu. 5 Walakini miili yetu ni kama miili ya ndugu zetu, na watoto wetu kama watoto wao; kumbe! Mnawatia utumwani wana wetu na binti zetu kuwa watumishi, na baadhi ya binti zetu wamekwisha kutiwa utumwani; wala hatuwezi kujiepusha na hayo; maana watu wengine wana mashamba yetu na mizabibu yetu. 6 Nami nilikasirika sana, niliposikia kilio chao, na maneno hayo. 7 Ndipo nikafanya shauri na nafsi yangu, nikagombana na wakuu na mashehe, nikawaambia, Mnatoza watu riba, kila mtu ndugu yake. Nikakutanisha mkutano mkubwa ili kushindana nao. 8 Nikawaambia, Sisi kwa kadiri ya uwezo wetu tumewakomboa ndugu zetu Wayahudi, waliouzwa kwa makafiri; na ninyi mnataka kuwauza ndugu zenu, tena kuwauza ili sisi tuwanunue? Wakanyamaza kimya, wasiweze kusema neno lo lote. 9 Tena nalisema, Neno hili mnalolitenda si jema; je! Haiwapasi ninyi kwenda katika kicho cha Mungu wetu, kwa sababu ya mashutumu ya makafiri adui zetu? 10 Na mimi pia, na ndugu zangu, na watumishi wangu, twawakopesha fedha na ngano ili kupata faida? Tafadhali na tuliache jambo hili la riba. 11 Naomba, warudishieni leo hivi mashamba yao, na mashamba yao ya mizabibu, na mashamba yao ya mizeituni, na nyumba zao, na lile fungu la mia la fedha, na la ngano, na la divai, na la mafuta, mnalowatoza. 12 Ndipo wakasema, Tutawarudishia, wala hatutataka kitu kwao; tutafanya hivyo, kama ulivyosema. Kisha nikawaita makuhani, nikawaapisha, ya kwamba watafanya kama ahadi hiyo. 13 Tena nikakung'uta nguo yangu, nikasema, Mungu na amkung'ute vivyo hivyo kila mtu nyumbani mwake, na kazini mwake, asiyeitimiza ahadi hiyo; naam, na akung'utwe vivyo hivyo, na kuwa hana kitu. Mkutano wote wakasema, Amina; wakamhimidi Bwana. Nao watu wakafanya kama ahadi hiyo. 14 Tena tangu wakati huo nilipowekwa kuwa liwali wao katika nchi ya Yuda, tangu mwaka wa ishirini hata mwaka wa thelathini na mbili wa Artashasta mfalme, yaani, miaka kumi na miwili, mimi na ndugu zangu hatukula chakula cha liwali. 15 Lakini maliwali wa kwanza walionitangulia, wakawalemea watu, wakawatwalia chakula na mvinyo, zaidi ya shekeli arobaini za fedha; tena watumwa wao nao wakatawala juu ya watu; lakini mimi sikufanya hivyo, kwa kuwa nalimcha Mungu. 16 Naam, hata kazi ya ukuta huu tena nikaishika sana, wala hatukununua mashamba; na watumishi wangu wote wakakusanyika huko kazini. 17 Pamoja na hayo wakawako mezani pangu, katika Wayahudi na mashehe, watu mia na hamsini, zaidi ya wale waliotujia kutoka kwa makafiri waliotuzunguka. 18 Basi, maandalio yaliyoandaliwa kwa siku moja yalikuwa ng'ombe mmoja, na kondoo wazuri sita; tena nikaandaliwa kuku, na mara moja katika siku kumi akiba ya mvinyo ya namna zote; wala kwa hayo yote sikukidai chakula cha liwali, kwa kuwa utumwa ulikuwa mzito juu ya watu hao. 19 Unikumbukie, Ee Mungu wangu, kwa mema, yote niliyowafanyia watu hawa.

Nehemia 6

1 Basi ikawa, walipoarifiwa Sanbalati, na Tobia, na Geshemu, Mwarabu na adui zetu hao wengine, kwamba nimeujenga ukuta, wala hayakusalia mavunjiko ndani yake; (ijapokuwa hata wakati ule sijaisimamisha milango katika malango); 2 Sanbalati na Geshemu wakatuma wajumbe kwangu, wakasema, Njoo, tukutane huko vijijini katika nchi tambarare ya Ono. Walakini wakakusudi kunifanyia mabaya. 3 Na mimi nikatuma wajumbe kwao, nikasema, Hii ni kazi kubwa ninayoifanya mimi, hata nisiweze kushuka; mbona kazi ikome, hapo ninapoiacha, niwashukie? 4 Nao wakaniletea maneno kama hayo mara nne; nikawajibu maneno kama yale. 5 Ndipo Sanbalati akamtuma kwangu mtumwa wake vile vile mara ya tano, na barua wazi mkononi mwake; 6 nayo yakaandikwa humo, Habari imeenea katika mataifa, naye Geshemu asema neno lilo hilo, ya kwamba wewe na Wayahudi mwakusudi kuasi; ndiyo sababu waujenga huo ukuta; nawe wataka kuwamiliki, ndivyo wasemavyo. 7 Nawe umewaweka manabii ili wakuhubirie huko Yerusalemu, kusema, Yuko mfalme katika Yuda; basi sasa ataarifiwa mfalme sawasawa na maneno haya. Njoo sasa basi, na tufanye shauri pamoja. 8 Ndipo mimi nikatuma kwake wajumbe, kusema, Hakukufanyika mambo kama hayo uyasemayo, lakini kwa moyo wako wewe mwenyewe umeyabuni. 9 Kwani hao wote walitaka kutuogofisha, wakisema, Italegea mikono yao katika kazi, isifanyike. Lakini sasa nitaitia mikono yangu nguvu. 10 Nikaingia nyumbani kwa Shemaya, mwana wa Delaya, mwana wa Mehetabeli, aliyekuwa amefungwa; naye akasema, Tukutane nyumbani mwa Mungu, ndani ya hekalu, tukaifunge milango ya hekalu; kwa maana watakuja kukuua; naam, wakati wa usiku watakuja kukuua. 11 Nami nikasema, Je! Mtu kama mimi nikimbie? Naye ni nani, akiwa kama nilivyo mimi, atakayeingia hekaluni ili kuponya maisha yake? Sitaingia. 12 Nikatambua, na tazama, siye Mungu aliyemtuma; lakini amefanya unabii huu kinyume changu; nao Tobia na Sanbalati ndio waliomwajiri. 13 Kwa sababu hii aliajiriwa, ili mimi niogope, nikafanye hivyo na kutenda dhambi, kisha wao wawe nazo habari mbaya, ili wanishutumie. 14 Uwakumbuke, Ee Mungu wangu, Tobia na Sanbalati sawasawa na hayo matendo yao, na yule nabii mke Noadia, na hao manabii waliosalia, waliotaka kuniogofya. 15 Basi huo ukuta ukamalizika siku ya ishirini na tano ya mwezi wa Eluli, katika muda wa siku hamsini na mbili. 16 Ikawa adui zetu wote waliposikia, ndipo makafiri wote waliotuzunguka wakaogopa, nao wakakata tamaa sana machoni pao wenyewe; maana waliitambua kazi hiyo ilivyotendwa na Mungu wetu. 17 Tena siku zile wakuu wa Yuda walimletea Tobia nyaraka nyingi, nazo nyaraka za Tobia zikawafikilia. 18 Kwa maana walikuwa watu wengi katika Yuda waliomwapia, kwa sababu alikuwa mkwewe Shekania, mwana wa Ara; naye Yehohanani mwanawe amemwoa binti Meshulamu, mwana wa Berekia. 19 Tena waliyanena mema yake mbele yangu, nayo maneno yangu humwambia yeye. Tobia naye akaniletea mimi nyaraka za kuniogofisha.

Nehemia 7

1 Ikawa, hapo ukuta ulipojengwa, na milango nimekwisha kuisimamisha, na mabawabu, na waimbaji, na Walawi, wamewekwa, 2 ndipo nilimwagiza ndugu yangu, Hanani, pamoja na yule Hanania, jemadari wa ngome, kuwa na amri juu ya Yerusalemu; kwa maana alikuwa mtu mwaminifu huyo, na mwenye kumcha Mungu kuliko wengi. 3 Nikawaambia, Yasifunguliwe malango ya Yerusalemu kabla halijachomoza jua; nao walinzi wangali wakisimama bado, waifunge milango, mkaikaze; kisha wekeni walinzi wa zamu wa hao wakaao Yerusalemu, kila mtu na zamu yake, na kila mtu kuielekea nyumba yake. 4 Basi mji ulikuwa wa nafasi nyingi, tena mkubwa; lakini watu waliomo walikuwa haba, wala nyumba hazijajengwa. 5 Mungu wangu akanitia moyoni mwangu, kwamba niwakusanye wakuu na mashehe, na watu, ili wahesabiwe kwa nasaba. Nikakiona kitabu cha vizazi vya hao waliokwea hapo kwanza, nikaona ya kwamba imeandikwa humo; 6 Hawa ndio wana wa wilaya, waliokwea kutoka katika ule uhamisho wa hao waliokuwa wamechukuliwa, ambao Nebukadreza, mfalme wa Babeli ,aliwachukua mateka,nao wakarudiYerusalemu na Yuda,kila mtu mjini kwake. 7 ndio hawa waliokuja pamoja na Zerubabeli, Yoshua, Nehemia, Seraya, Reelaya, Nahamani, Mordekai, Bilshani, Mispari, Bigwai, Rehumu, na Baana. Hii ndiyo hesabu ya wanaume wa watu wa Israeli; 8 Wana wa Paroshi, elfu mbili mia moja sabini na wawili. 9 Wana wa Shefatia, mia tatu sabini na wawili. 10 Wana wa Ara mia sita hamsini na wawili. 11 Wana wa Pahath-Moabu, wa wana wa Yeshua na Yoabu, elfu mbili mia nane na kumi na wanane. 12 Wana wa Elamu, elfu moja mia mbili hamsini na wanne. 13 Wana wa Zatu, mia nane arobaini na watano. 14 Wana wa Zakai, mia saba na sitini. 15 Wana wa Binui, mia sita arobaini na wanane. 16 Wana wa Bebai, mia sita ishirini na wanane. 17 Wana wa Azgadi, elfu mbili mia tatu ishirini na wawili. 18 Wana wa Adonikamu, mia sita sitini na saba. 19 Wana wa Bigwai, elfu mbili sitini na saba. 20 Wana wa Adini, mia sita hamsini na watano. 21 Wana wa Ateri, wa Hezekia, tisini na wanane. 22 Wana wa Hashumu, mia tatu ishirini na wanane. 23 Wana wa Besai, mia tatu ishirini na wanne. 24 Wana wa Harifu, mia moja na kumi na wawili. 25 Wana wa Gibeoni, tisini na watano. 26 Watu wa Bethlehemu na Netofa, mia na themanini na wanane. 27 Watu wa Anathothi, mia na ishirini na wanane. 28 Watu wa Beth-Azmawethi, arobaini na wawili. 29 Watu wa Kiriath-Yearimu, na Kefira, na Beerothi, mia saba arobaini na watatu. 30 Watu wa Rama na Geba, mia sita na ishirini na mmoja. 31 Watu wa Mikmashi, mia moja na ishirini na wawili. 32 Watu wa Betheli na Ai, mia moja ishirini na watatu. 33 Watu wa Nebo, hamsini na wawili. 34 Wana wa Elamu wa pili, elfu moja mia mbili hamsini na wanne. 35 Wana wa Harimu, mia tatu na ishirini. 36 Wana wa Yeriko, mia tatu arobaini na watano. 37 Wana wa Lodi, na Hadidi, na Ono, mia saba ishirini na mmoja. 38 Watu wa Senaa, elfu tatu mia kenda na thelathini. 39 Makuhani; Wana wa Yedaya, wa mbari ya Yeshua, mia kenda sabini na watatu. 40 Wana wa Imeri, elfu moja hamsini na wawili. 41 Wana wa Pashuri, elfu moja mia mbili arobaini na saba. 42 Wana wa Harimu, elfu moja na kumi na saba. 43 Walawi; Wana wa Yeshua, wa Kadmieli wa wana wa Hodavia, sabini na wanne. 44 Waimbaji; Wana wa Asafu, mia moja arobaini na wanane. 45 Mabawabu; Wana wa Shalumu, wana wa Ateri, wana wa Talmoni, wana wa Akubu, wana wa Hatita, wana wa Shobai, mia moja thelathini na wanane. 46 Wanethini; wana wa Siha, wana wa Hasufa, wana wa Tabaothi; 47 wana wa Kerosi, wana wa Siaha, wana wa Padoni; 48 wana wa Lebana, wana wa Hagaba, wana wa Salmai; 49 wana wa Hanani, wana wa Gideli, wana wa Gahari; 50 wana wa Reaya, wana wa Resini, wana wa Nekoda; 51 wana wa Gazamu, wana wa Uza, wana wa Pasea; 52 wana wa Besai wana wa Meunimu, wana wa Nefusimu; 53 wana wa Bakbuki, wana wa Hakufa, wana wa Harhuri; 54 wana wa Basluthi, wana wa Mehida, wana wa Harsha; 55 wana wa Barkosi, wana wa Sisera, wana wa Tema; 56 wana wa Nesia, wana wa Hatifa. 57 Akina watumwa wa Sulemani; Wana wa Sotai, wana wa Soferethi, wana wa Peruda; 58 wana wa Yaala, wana wa Darkoni, wana wa Gideli; 59 wana wa Shefatia, wana wa Hatili, wana wa Pokereth-Sebaimu, wana wa Amoni. 60 Wanethini wote, pamoja na akina watumwa wa Sulemani, walikuwa mia tatu tisini na wawili. 61 Na hawa ndio watu waliokwea kutoka Tel-mela, na Tel-harsha, na Kerubu, na Adani, na Imeri; walakini hawakuweza kuonyesha mbari za baba zao, wala kizazi chao, kwamba walikuwa wa Israeli; 62 Wana wa Delaya, wana wa Tobia, wana wa Nekoda, mia sita na arobaini na wawili. 63 Tena katika makuhani; Wana wa Habaya, wana wa Hakosi, wana wa Barzilai, yule aliyeoa mmojawapo binti Barzilai, Mgileadi, akaitwa kwa jina lao. 64 Hao waliitafuta orodha yao miongoni mwa wale waliohesabiwa kwa nasaba, wasionekane; kwa hiyo walihesabiwa kuwa na unajisi. 65 Na huyo Tirshatha akawaambia kwamba wasile katika vile vitu vitakatifu sana, hata atakaposimama kuhani mwenye Urimu na Thumimu. 66 Basi hilo kusanyiko lote zima, jumla yake ilikuwa watu arobaini na mbili elfu na mia tatu na sitini, 67 tena zaidi ya hao, kulikuwa na watumishi wao waume kwa wake, ambao walikuwa elfu saba na mia tatu na thelathini na saba; kisha walikuwa na waimbaji waume kwa wake mia mbili arobaini na watano. 68 Farasi zao walikuwa mia saba thelathini na sita; nyumbu zao, mia mbili arobaini na watano; 69 ngamia zao, mia nne thelathini na watano; punda zao, elfu sita na mia saba na ishirini. 70 Na baadhi ya wakuu wa mbari za mababa walitoa mali kwa ajili ya kazi hii. Yule Tirshatha akatoa kwa ajili ya hazina darkoni za dhahabu elfu moja ,na mabakuli hamsini , na mavazi ya makuhani mia tano na thelathini. 71 Na baadhi ya wakuu wa mbari za mababa wakatoa, na kutia katika hazina ya kazi hiyo, darkoni za dhahabu ishirini elfu, na mane za fedha elfu mbili na mia mbili. 72 Na mabaki ya watu wakatoa darkoni za dhahabu ishirini elfu, na mane za fedha elfu mbili, na mavazi ya makuhani sitini na saba. 73 Hivyo makuhani, na Walawi, na mabawabu, na waimbaji, na baadhi ya watu, na Wanethini, na Israeli wote, wakakaa mijini mwao. Hata ulipowadia mwezi wa saba, wana wa Islaeli walikuwa wakikaa katika miji yao.

Nehemia 8

1 Na watu wote wakakusanyika kama mtu mmoja katika uwanja uliokuwa mbele ya lango la maji; wakamwambia Ezra, mwandishi, akilete kitabu cha torati ya Musa, Bwana aliyowaamuru Israeli. 2 Naye Ezra, kuhani, akaileta torati mbele ya kusanyiko, la wanaume na wanawake, na wote walioweza kusikia na kufahamu, siku ya kwanza na mwezi wa saba. 3 Akasoma humo mbele ya uwanja uliokuwa ukikabili lango la maji, tangu mapambazuko hata adhuhuri, mbele ya hao wanaume na wanawake, na wale walioweza kufahamu; na masikio ya watu wote yakasikiliza kitabu cha torati. 4 Naye Ezra, kuhani, akasimama juu ya mimbari ya mti, waliyokuwa wameifanya kwa kusudi hilo; na karibu naye wakasimama Matithia, na Shema, na Anaya, na Uria, na Hilkia, na Maaseya, mkono wake wa kuume; na mkono wake wa kushoto, Pedaya, na Misbaeli, na Malkiya, na Hashumu, na Hashbadani, na Zekaria, na Meshulamu. 5 Ezra akakifunua kitabu machoni pa watu wote; (maana alikuwa juu ya watu wote); na hapo alipokifungua, watu wote walisimama; 6 Ezra akamhimidi Bwana, Mungu Mkuu. Nao watu wote wakaitika, Amina, Amina, pamoja na kuinua mikono yao; kisha wakainama vichwa vyao, wakamsujudu Bwana kifudifudi. 7 Tena Yeshua, na Bani, na Sherebia, na Yamini, na Akubu, na Shabethai, na Hodai, na Maaseya, na Kelita, na Azaria, na Yozabadi, na Hanani, na Pelaya, nao ni Walawi, wakawafahamisha watu torati; na watu wakasimama mahali pao. 8 Nao wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa. 9 Naye Nehemia, ndiye aliyekuwa Tirshatha, na Ezra kuhani, mwandishi, na Walawi waliowafundisha watu, wakawaambia watu wote, Siku hii ni takatifu kwa Bwana, Mungu wenu; msiomboleze wala msilie. Maana watu wote walilia, walipoyasikia maneno ya torati. 10 Kisha akawaambia, Enendeni zenu, mle kilichonona, na kunywa kilicho kitamu, tena mpelekeeni sehemu yeye asiyewekewa kitu; maana siku hii ni takatifu kwa Bwana wetu; wala msihuzunike; kwa kuwa furaha ya Bwana ni nguvu zenu. 11 Hivyo Walawi wakawatuliza watu wote, wakasema, Nyamazeni, kwa maana siku hii ni takatifu; wala msihuzunike. 12 Na watu wote wakaenda zao kula na kunywa, na kuwapelekea watu sehemu, na kufanya furaha nyingi, kwa sababu walikuwa wameyafahamu maneno yale waliyohubiriwa. 13 Hata siku ya pili wakuu wa mbari za mababa za watu wote, na makuhani, na Walawi, wakamkusanyikia Ezra, mwandishi, ili wapate kuyasikiliza maneno ya torati. 14 Wakaona ya kuwa imeandikwa katika torati, jinsi Bwana alivyoamuru kwa mkono wa Musa, ya kwamba wana wa Israeli wakae katika vibanda, katika sikukuu ya mwezi wa saba; 15 na ya kwamba wahubiri na kutangaza katika miji yao yote, na katika Yerusalemu, kusema, Enendeni mlimani, mkalete matawi ya mzeituni, na matawi ya mzeituni-mwitu, na matawi ya mihadasi, na matawi ya mitende, na matawi ya miti minene, ili kufanya vibanda, kama ilivyoandikwa. 16 Basi watu wote wakatoka, wakayaleta, wakajifanyizia vibanda, kila mtu juu ya dari ya nyumba yake, na katika nyua zao, na katika nyua za nyumba ya Mungu, na katika uwanja wa lango la maji, na katika uwanja wa lango la Efraimu. 17 Na mkutano wote wa watu, waliorudi kutoka nchi ya uhamisho wao, wakafanyiza vibanda, wakakaa katika vibanda hivyo; maana tokea siku za Yoshua, mwana wa Nuni, hata siku ile, wana wa Israeli hawakufanya hivyo. Pakawa na furaha kubwa sana. 18 Tena siku baada ya siku, tangu siku ya kwanza hata siku ya mwisho, akasoma katika kitabu cha torati ya Mungu. Wakafanya sikukuu muda wa siku saba; na siku ya nane palikuwa na kusanyiko la makini, kama ilivyoagizwa.

Nehemia 9

1 Hata siku ya ishirini na nne ya mwezi huo wana wa Israeli wakawa wamekusanyika, wakifunga, wenye kuvaa magunia, na kujitia udongo vichwani. 2 Waliokuwa wa wazao wa Israeli wakajitenga na wageni wote, wakasimama, wakaziungama dhambi zao, na maovu ya baba zao. 3 Basi wakasimama mahali pao, wakasoma katika kitabu cha torati ya Bwana, Mungu wao, muda wa robo ya siku; na robo nyingine wakaungama, wakamwabudu Bwana, Mungu wao. 4 Ndipo wakasimama madarajani pa Walawi, Yeshua, na Bani, na Kadmieli, na Shebania, na Buni, na Sherebia, na Bani, na Kenani, wakamlilia Bwana, Mungu wao, kwa sauti kuu. 5 Ndipo Walawi, Yeshua na Kadmieli, na Bani, na Hashabneya, na Sherebia, na Hodia, na Shebania, na Pethahia, wakasema, Simameni, mkamhimidi Bwana, Mungu wenu, tangu milele na hata milele. Na lihimidiwe jina lako tukufu, lililotukuka kuliko baraka zote na sifa zote. 6 Ezra akasema, Wewe ndiwe Bwana, wewe peke yako; wewe ulifanya mbingu, mbingu za mbingu, pamoja na jeshi lake lote, dunia na vyote vilivyomo, bahari na vitu vyote vilivyomo, nawe unavihifadhi vitu hivi vyote; na jeshi la mbinguni lakusujudu wewe. 7 Wewe ndiwe Bwana, Mungu, uliyemchagua Abramu, na kumtoa katika Uri wa Wakaldayo, na kumpa jina la Ibrahimu; 8 nawe ukauona moyo wake kuwa mwaminifu mbele zako, ukafanya agano naye, kumpa nchi ya Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Myebusi, na Mgirgashi, naam, kuwapa wazao wake; nawe umeyafikiliza maneno yako, kwa kuwa ndiwe mwenye haki. 9 Tena uliyaona mateso ya baba zetu katika Misri, ukakisikia kilio chao, huko kando ya bahari ya Shamu; 10 nawe ukaonyesha ishara nyingi na mambo ya ajabu juu ya Farao, na juu ya watumishi wake wote, na juu ya watu wote wa nchi yake; kwa maana ulijua ya kuwa waliwatenda kwa kutakabari; ukajipatia jina kama vile ilivyo leo. 11 Nawe uliipasua bahari mbele yao, hata wakapita katikati ya bahari katika nchi kavu; na wale waliokuwa wakiwafuatia ukawatupa vilindini, mfano wa jiwe katika maji makuu. 12 Zaidi ya hayo ukawaongoza kwa nguzo ya wingu mchana; na kwa nguzo ya moto usiku; ili kuwapa mwanga katika njia iliyowapasa kuiendea. 13 Tena ulishuka juu ya mlima Sinai, ukasema nao toka mbinguni, ukawapa hukumu za haki, na sheria za kweli, na amri nzuri na maagizo; 14 ukawajulisha sabato yako takatifu, na kuwaagiza maagizo, na amri, na sheria, kwa mkono wa mtumishi wako, Musa. 15 Ukawapa chakula toka mbinguni, kwa ajili ya njaa yao, na kwa ajili yao ukaleta maji kutoka mwambani, kwa sababu ya kiu yao, ukawaamuru kwamba waingie katika nchi na kuimiliki, ambayo umeinua mkono wako kuwapa. 16 Lakini wao na baba zetu wakatakabari, wakafanya shingo zao kuwa ngumu, wala hawakuzisikiliza amri zako, 17 ila wakakataa kutii, wala hawakuyakumbuka maajabu yako, uliyoyafanya kati yao; lakini wakafanya shingo zao kuwa ngumu, na katika kuasi kwao wakaweka jemadari, ili wairudie hali ya utumwa; lakini wewe u Mungu, uliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema, basi hukuwaacha. 18 Naam, hata walipojifanyia ndama ya kusubu, na kusema, Huyu ndiye Mungu wako aliyekupandisha kutoka Misri, tena walipokuwa wamefanya machukizo makuu; 19 hata hivyo wewe kwa wingi wa rehema zako hukuwaacha jangwani; nguzo ya wingu haikuwaondokea wakati wa mchana, ili kuwaongoza njiani; wala nguzo ya moto haikuondoka wakati wa usiku, ili kuwapa mwanga na kuwaonyesha njia watakayoiendea. 20 Ukawapa na roho yako mwema ili kuwaelimisha, wala hukuwanyima mana vinywani mwao, tena ukawapa maji kwa ajili ya kiu yao. 21 Naam, muda wa miaka arobaini uliwaruzuku jangwani, wasihitaji kitu; nguo zao hazikuchakaa, wala miguu yao haikuvimba. 22 Pamoja na hayo ukawapa falme na taifa za watu, ulizowagawia sawasawa na mafungu yao; hivyo wakaimiliki nchi ya Sihoni, naam, nchi yake mfalme wa Heshboni, na nchi ya Ogu, mfalme wa Bashani. 23 Watoto wao nao uliwaongeza kama nyota za mbinguni, ukawaingiza katika nchi ile, uliyowaambia baba zao kuwa wataingia kuimiliki. 24 Basi wale watoto wakaingia wakaimiliki nchi, nawe ukawatiisha wenyeji wa nchi mbele yao, ndio Wakanaani, ukawatia mikononi mwao, pamoja na wafalme wao, na watu wa nchi, wawatende kama wapendavyo. 25 Wakaitwaa miji yenye boma, na nchi yenye neema, wakazitamalaki nyumba zilizojaa vitu vyema, birika zilizochimbwa, mizabibu, na mizeituni, na miti mingi yenye matunda; hivyo wakala, wakashiba, wakanenepa, wakajifurahisha katika wema wako mwingi. 26 Walakini hawakukutii, wakakuasi, wakaitupa sheria yako nyuma yao, wakawaua manabii wako walioshuhudu juu yao wapate kuwarejeza kwako; wakatenda machukizo makuu. 27 Kwa sababu hiyo ukawatia katika mikono ya adui zao, waliowasumbua; na wakati wa shida yao, walipokulilia, uliwasikia kutoka mbinguni; na kwa wingi wa rehema zako ukawapa waokozi waliowaokoa katika mikono ya adui zao. 28 Lakini walipokuwa wamekwisha kustarehe, walitenda mabaya tena mbele zako; kwa hiyo ukawaacha katika mikono ya adui zao, nao wakawatawala; hata hivyo waliporejea na kukulilia, uliwasikia toka mbinguni; ukawaokoa mara nyingi kwa rehema zako; 29 ukawashuhudia ili uwarudishe tena katika sheria yako; lakini walitakabari, wasizisikilize amri zako, bali wakazihalifu hukumu zako, (ambazo mtu akizitenda ataishi katika hizo), nao wakayaondoa mabega yao, wakafanya shingo zao kuwa ngumu, wasitake kusikiliza. 30 Lakini miaka mingi ukachukuliana nao, nawe ukawashuhudia kwa roho yako kwa vinywa vya manabii wako; wao wasitake kusikiliza; kwa hiyo ukawatia katika mikono ya watu wa nchi. 31 Ila kwa rehema zako nyingi hukuwakomesha kabisa, wala kuwaacha; kwa maana wewe u Mungu mwenye neema, mwenye rehema. 32 Basi sasa, Ee Mungu, mkuu, mwenye uweza, Mungu wa kuogofya, mwenye kushika maagano na rehema, mashaka yote yaliyotupata sisi, wafalme wetu, na wakuu wetu, na makuhani wetu, na manabii wetu, na baba zetu, na watu wako wote, tangu zamani za wafalme wa Ashuru hata leo, na yasihesabiwe kuwa ni madogo. 33 Lakini wewe u mwenye haki, katika hayo yote yaliyotupata; maana wewe umetenda yaliyo kweli, lakini sisi tumetenda yaliyo mabaya; 34 na wafalme wetu, na wakuu wetu, na makuhani wetu, na baba zetu, hawakuishika sheria yako, wala hawakuzisikiliza amri zako na shuhuda zako, ulizowashuhudia. 35 Kwa kuwa hawakukutumikia wewe katika ufalme wao, na katika wema wako mkuu uliowapa, na katika nchi ile kubwa yenye neema uliyowapa mbele yao, wala hawakughairi na kuyaacha mabaya yao. 36 Tazama, sisi hapa tu watumwa leo, na katika habari ya nchi hii uliyowapa baba zetu, wapate kula matunda yake na mema yake, tazama, sisi hapa tu watumwa ndani yake. 37 Nayo yawapatia faida nyingi wafalme uliowaweka juu yetu kwa sababu ya dhambi zetu; tena wana mamlaka juu ya miili yetu, na juu ya wanyama wetu, kadiri wapendavyo, nasi tu katika dhiki kuu. 38 Na kwa sababu ya hayo yote sisi twafanya agano la hakika, na kuliandika; na wakuu wetu, na Walawi wetu, na makuhani wetu, wanalitilia muhuri.

Nehemia 10

1 Basi hawa ndio waliotia muhuri; Nehemia, ndiye Tirshatha, mwana wa Hakalia, na Sedekia; 2 Seraya, Azaria, Yeremia; 3 Pashuri, Amaria, Malkiya; 4 Hamshi, Shekania, Maluki; 5 Harimu, Meremothi, Obadia; 6 Danieli, Ginethoni, Baruki; 7 Meshulamu, Abiya, Miyamini; 8 Maazia, Bilgai, Shemaya; hao ndio waliokuwa makuhani. 9 Na Walawi; ndio, Yeshua, mwana wa Azania, Binui wa wana wa Henadadi, Kadmieli; 10 na ndugu zao, Shebania, Hodia, Kelita, Pelaya, Hanani; 11 Mika, Rehobu, Hashabia; 12 Zakuri, Sherebia, Shebania; 13 Hodia, Bani, Beninu; 14 Na wakuu wa watu; Paroshi, Pahath-Moabu, Elamu, Zatu, Bani; 15 Buni, Azgadi, Bebai; 16 Adonikamu, Bigwai, Adini; 17 Ateri, Hezakia, Azuri; 18 Hodia, Hashumu, Besai; 19 Harifu, Anathothi, Nobai; 20 Magpiashi, Meshulamu, Heziri; 21 Meshezabeli, Sadoki, Yadua; 22 Pelatia, Hanani, Anaya; 23 Hoshea, Hanania, Hashubu; 24 Haloheshi, Pilha, Shobeki; 25 Rehumu, Hashabna, Maaseya; 26 Ahia, Hanani, Anani; 27 Maluki, Harimu, na Baana. 28 Na watu waliosalia, makuhani, Walawi, mabawabu, waimbaji, Wanethini, na hao wote waliojitenga katika watu wa nchi kwa torati ya Mungu; wake zao, na wana wao, na binti zao, kila mwenye maarifa na akili; 29 wakaambatana na ndugu zao, wakuu wao, nao wakaingia katika laana na kiapo, ya kuwa wataiendea torati ya Mungu, iliyotolewa kwa mkono wa Musa, mtumishi wa Mungu, na kuziangalia, na kuzitenda, amri zote za Bwana, Bwana wetu, na hukumu zake na sheria zake; 30 wala tusiwaoze watu wa nchi binti zetu, wala kuwatwalia wana wetu binti zao; 31 tena watu wa nchi wakitembeza biashara, au chakula cho chote, siku ya sabato, tusinunue kwao siku ya sabato, au siku takatifu; tena kwamba tuuache mwaka wa saba, na madai ya kila deni. 32 Tena tukajifanyia maagizo, kujitoza mwaka kwa mwaka theluthi ya shekeli kwa huduma ya nyumba ya Mungu wetu; 33 kwa mikate ya wonyesho, na kwa sadaka ya unga ya daima, na kwa sadaka ya kuteketezwa ya daima, ya sabato, na ya siku za mwezi mpya, na ya sikukuu, tena kwa vitu vile vitakatifu, na kwa sadaka za dhambi, za kuwafanyia Israeli upatanisho, na kwa ajili ya kazi yote ya nyumba ya Mungu wetu. 34 Kisha tukapiga kura, makuhani, na Walawi, na watu, juu ya matoleo ya kuni, ili kuzileta nyumbani kwa Mungu wetu, kwa kadiri ya mbari za baba zetu, kwa nyakati zilizoamriwa, mwaka kwa mwaka, kukoka moto madhabahuni mwa Bwana, Mungu wetu, kama ilivyoandikwa katika torati; 35 tena kuleta malimbuko ya ardhi yetu, na malimbuko ya matunda yote ya miti ya namna zote, mwaka kwa mwaka, nyumbani kwa Bwana; 36 tena wazaliwa wa kwanza wa wana wetu, na wa wanyama wetu, kama ilivyoandikwa katika torati, na wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe zetu na kondoo zetu, ili kuwaleta nyumbani mwa Mungu wetu, kwa makuhani watumikao nyumbani mwa Mungu wetu; 37 tena tuyalete malimbuko ya unga wetu, na sadaka zetu za kuinuliwa, na matunda ya miti ya namna zote, mvinyo, na mafuta, kwa makuhani, hapo vyumbani kwa nyumba ya Mungu wetu; na zaka za ardhi yetu kwa Walawi; kwa kuwa hao Walawi wazitwaa zaka mijini mwote mwa kulima kwetu. 38 Naye kuhani, mwana wa Haruni, atakuwako pamoja na Walawi, watwaapo zaka Walawi; nao Walawi wataipandisha zaka ya hizo zaka nyumbani kwa Mungu wetu, vyumbani, katika nyumba ya hazina. 39 Kwa kuwa wana wa Israeli na wana wa Lawi wataleta sadaka ya kuinuliwa ya nafaka, na mvinyo, na mafuta, vyumbani, kwa kuwa ndimo vilimo vyombo vya patakatifu, na makuhani watumikao, na mabawabu, na waimbaji; wala sisi hatutaiacha nyumba ya Mungu wetu.

Nehemia 11

1 Basi, wakuu wa watu walikuwa wakikaa Yerusalemu; nao watu waliosalia wakapiga kura, ili katika watu kumi kumleta mmoja akae ndani ya Yerusalemu mji mtakatifu, na wale kenda wakae mijini. 2 Na hao watu wakawabariki wote waliojitoa kwa hiari wakae Yerusalemu. 3 Basi hawa ndio wakuu wa jimbo waliokaa Yerusalemu; ila mijini mwa Yuda wakakaa kila mtu katika milki yake mijini mwao, yaani, Israeli, makuhani, na Walawi, na Wanethini, na akina watumwa wa Sulemani. 4 Tena wakakaa Yerusalemu wengine wa wana wa Yuda, na wengine wa wana wa Benyamini. Wa wana wa Yuda; Athaya, mwana wa Uzia, mwana wa Zekaria, mwana wa Amaria, mwana wa Shefatia, mwana wa Mahalaleli, wa wana wa Peresi; 5 na Maaseya, mwana wa Baruki, mwana wa Kolhoze, mwana wa Hazaya, mwana wa Adaya, mwana wa Yoyaribu, mwana wa Zekaria, Mshelani. 6 Wana wa Peresi wote waliokaa Yerusalemu walikuwa watu mia nne sitini na wanane, mashujaa. 7 Na wana wa Benyamini ndio hawa; Salu, mwana wa Meshulamu, mwana wa Yoedi, mwana wa Pedaya, mwana wa Kolaya, mwana wa Maaseva, mwana wa Ithieli, mwana wa Yeshaya. 8 Na baada yake Gabai, Salai, watu mia kenda ishirini na wanane. 9 Na Yoeli, mwana wa Zikri, alikuwa msimamizi wao; na Yuda, mwana wa Hasenua, alikuwa wa pili juu ya mji. 10 Wa makuhani; Yedaya, Yoyaribu, Yakini, 11 na Seraya, mwana wa Hilkia, mwana wa Meshulamu, mwana wa Sadoki, mwana wa Merayothi, mwana wa Ahitubu, msimamizi wa nyumba ya Mungu, 12 na ndugu zao waliofanya kazi ya nyumbani, watu mia nane ishirini na wawili; na Adaya, mwana wa Yerohamu, mwana wa Pelalia, mwana wa Amzi, mwana wa Zekaria, mwana wa Pashuri, mwana wa Malkiya, 13 na ndugu zake, wakuu wa mbari za mababa, watu mia mbili arobaini na wawili; na Maasai, mwana wa Azareli, mwana wa Azai, mwana wa Meshilemothi, mwana wa Imeri, 14 na ndugu zao, waume mashujaa, watu mia na ishirini na wanane; na msimamizi wao alikuwa Zabdieli, mmojawapo wa hao wakuu. 15 Na wa Walawi; Shemaya, mwana wa Hashubu, mwana wa Azrikamu, mwana wa Hashabia, mwana wa Buni; 16 na Shabethai na Yozabadi, wa wakuu wa Walawi, walioisimamia kazi ya nje ya nyumba ya Mungu; 17 na Matania, mwana wa Mika, mwana wa Zikri, mwana wa Asafu, mkuu mwenye kuanzisha shukrani katika sala, na Bakbukia, wa pili wake miongoni mwa nduguze; na Obadia, mwana wa Shemaya, mwana wa Galali, mwana wa Yeduthuni. 18 Walawi wote waliokaa katika mji mtakatifu walikuwa watu mia mbili themanini na wanne. 19 Pamoja na hao, mabawabu; Akubu, Talmoni, na ndugu zao waliolinda malangoni, walikuwa watu mia na sabini na wawili. 20 Na Israeli waliosalia, katika hao makuhani, na Walawi, walikuwamo mijini mwote mwa Yuda, kila mtu katika milki yake. 21 Lakini Wanethini walikuwa wakikaa Ofeli; na juu ya Wanethini walikuwa Siha na Gishpa. 22 Naye msimamizi wa Walawi huko Yerusalemu, ni Uzi, mwana wa Bani, mwana wa Hashabia, mwana wa Matania, mwana wa Mika, wa wana wa Asafu, hao waimbaji, alikuwa juu ya kazi ya nyumba ya Mungu. 23 Kwa kuwa palikuwa na amri ya mfalme juu yao, na agizo la hakika walilowekewa waimbaji, kama ilivyohusika na kila siku. 24 Na Pethahia, mwana wa Meshezabeli, wa wana wa Zera, mwana wa Yuda, alikuwa wakili wa mfalme kwa habari ya mambo yote ya watu. 25 Na katika habari za vijiji na mashamba yake; wengine wa wana wa Yuda walikuwa wakikaa Kiriath-arba na vijiji vyake, na katika Diboni na vijiji vyake, na Yekabzeeli na vijiji vyake; 26 na katika Yeshua, na Molada, na Beth-peleti; 27 na Hazar-shuali, na Beer-sheba na vijiji vyake; 28 na katika Siklagi, na Mekona na vijiji vyake; 29 na katika Enrimoni, na Sora, na Yarmuthi; 30 Zanoa, Adulamu na vijiji vyake, Lakishi na mashamba yake, Azeka na vijiji vyake. Hivyo wakatua toka Beer-sheba mpaka bonde la Hinomu. 31 Wana wa Benyamini nao walikuwa wakikaa Geba, na Mikmashi, na Aiya, na Beth-eli na vijiji vyake; 32 Anathothi, Nobu, Anania; 33 Hazori, Rama, Gitaimu; 34 Hadidi, Seboimu, Nebalati; 35 Lodi, na Ono, bonde la Wakarashi. 36 Na wa Walawi, wengine walikaa katika Yuda na wengine katika Benyamini.

Nehemia 12

1 Basi, hawa ndio makuhani na Walawi waliopanda na Zerubabeli, mwana wa Shealueli, na Yoshua; Seraya, Yeremia, Ezra; 2 Amaria, Maluki, Hatushi; 3 Shekania, Harimu, Meremothi; 4 Ido, Ginethoni, Abia; 5 Miyamini, Maazia, Bilgai; 6 Shemaya, Yoyaribu, Yedaya; 7 Salu, Amoki, Hilkia, Yedaya. Hawa walikuwa wakuu wa makuhani na ndugu zao siku za Yoshua. 8 Tena Walawi; Yeshua, Binui, Kadmieli, Sherebia, Yuda, na Matania, aliyekuwa juu ya shukrani, yeye na ndugu zake. 9 Tena Bakbukia na Uno, ndugu zao, kuwaelekea kwa zamu. 10 Naye Yoshua akamzaa Yoyakimu, Yoyakimu akamzaa Eliashibu, Eliashibu akamzaa Yoyada, 11 Yoyada akamzaa Yohana, Yohana akamzaa Yadua. 12 Na siku za Yoyakimu wakawako makuhani, wakuu wa mbari za mababa; wa Seraya, Meraya; wa Yeremia, Hanania; 13 wa Ezra, Meshulamu; wa Amaria, Yehohanani; 14 wa Maluki, Yonathani; wa Shekania, Yusufu; 15 wa Harimu, Adna; wa Meremothi, Helkai; 16 wa Ido, Zekaria; wa Ginethoni, Meshulamu; 17 wa Abia, Zikri; wa Miyamini; wa Maazia, Piltai; 18 wa Bilgai, Shamua; wa Shemaya, Yehonathani; 19 wa Yoyaribu, Matenai; wa Yedaya, Uzi; 20 wa Salu, Kalai; wa Amoki, Eberi; 21 wa Hilkia, Hashabia; wa Yedaya, Nethaneli. 22 Walawi siku za Eliashibu, na Yoyada, na Yohana, na Yadua, wameandikwa wakuu wa mbari za mababa; tena na makuhani; hata siku za kumiliki kwake Dario, Mwajemi. 23 Wana wa Lawi, wakuu wa mbari za mababa, wameandikwa katika kitabu cha tarehe, hata siku za Yohana mwana wa Eliashibu. 24 Nao wakuu wa Walawi; Hashabia, Sherebia, Yeshua, Binui, Kadmieli, na ndugu zao kuwaelekea, ili kusifu na kushukuru, kama amri ya Daudi, mtu wa Mungu, zamu kwa zamu. 25 Matania, Bakbukia, Obadia, Meshulamu, Talmoni, na Akubu, walikuwa mabawabu, wa kulinda nyumba za hazina penye malango. 26 Hao walikuwapo siku za Yoyakimu, mwana ya Yoshua, mwana wa Yosadaki, na siku za Nehemia, liwali, na Ezra, kuhani, mwandishi. 27 Basi, walipouweka wakfu ukuta wa Yerusalemu wakawatafuta Walawi katika mahali pao pote, ili kuwaleta Yerusalemu, wapate kufanya wakfu pamoja na furaha, na kwa shukrani, na kwa kuimba, kwa matoazi, vinanda na vinubi. 28 Waimbaji wakakusanyika kutoka uwanda na viunga vya Yerusalemu, na kutoka vijiji vya Wanetofathi; 29 tena toka Beth-gilgali, na toka mashamba ya Geba na Azmawethi; kwa maana waimbaji hao walikuwa wamejijengea vijiji katika viunga vya Yerusalemu. 30 Makuhani na Walawi wakajitakasa, nao wakawatakasa watu, na malango, na ukuta. 31 Ndipo nikawapandisha wakuu wa Yuda juu ya ukuta, nikawaagiza mikutano mikubwa miwili ya hao walioshukuru, na kuandamana; mmoja uende kwa kuume ukutani kuliendea lango la jaa; 32 na baada yao wakaenda Hoshaya, na nusu ya wakuu wa Yuda, 33 na Azaria, na Ezra, na Meshulamu, 34 na Yuda, na Benyamini, na Shemaya, na Yeremia, 35 na baadhi ya makuhani wenye baragumu; Zekaria, mwana wa Yonathani, mwana wa Shemaya, mwana wa Matania, mwana wa Mikaya, mwana wa Zakuri, mwana wa Asafu; 36 na ndugu zake, Shemaya, Azareli, Milalai, Gilalai, Maai, Nethaneli, Yuda, na Hanani, wenye vinanda vya Daudi mtu wa Mungu; Ezra, mwandishi, akawatangulia; 37 na kwa lango la chemchemi, wakienda moja kwa moja mbele yao, wakapanda madaraja ya mji wa Daudi, uinukapo ukuta, juu ya nyumba ya Daudi, mpaka lango la maji upande wa mashariki. 38 Na mkutano wa pili wao wenye kushukuru wakaenda kuwalaki, na mimi nikafuata nyuma yao, pamoja na nusu ya watu, ukutani juu ya mnara wa tanuu, mpaka ule ukuta mpana; 39 na juu ya lango la Efraimu, na kupita lango la kale, na lango la samaki, na mnara wa Hananeli, na mnara wa Hamea, mpaka lango la kondoo; nao wakasimama hapo langoni pa gereza. 40 Ndivyo walivyosimama mikutano miwili yao walioshukuru nyumbani mwa Mungu, na mimi, na nusu ya mashehe pamoja nami; 41 na makuhani, Eliakimu, Maaseya, Miyamini, Mikaya, Elioenai, Zekaria na Hanania, wenye baragumu; 42 na Maaseya, na Shemaya, na Eleazari, na Uzi, na Yehohanani, na Malkiya, na Elamu, na Ezeri. Waimbaji wakaimba kwa sauti kuu, wenye Yezrahia kuwa msimamizi wao. 43 Wakatoa dhabihu nyingi siku ile, wakafurahi; kwa kuwa Mungu amewafurahisha furaha kuu; na wanawake pia na watoto wakafurahi; hata ikasikiwa mbali sana furaha hiyo ya Yerusalemu. 44 Na siku hiyo watu wakaagizwa juu ya vyumba vya hazina, kwa sadaka za kuinuliwa, na kwa malimbuko, na kwa zaka, ili kuzikusanya, kwa kadiri ya mashamba ya miji, sehemu zilizoamriwa katika torati za makuhani, na Walawi; kwa maana Yuda waliwafurahia makuhani na Walawi waliotumika. 45 Wakauangalia ulinzi wa Mungu wao, na ulinzi wa kutakasika, na hao waimbaji na mabawabu vile vile, sawasawa na amri ya Daudi, na ya Sulemani mwanawe. 46 Kwa kuwa siku za Daudi zamani, Asafu alikuwa mkuu wa waimbaji, na juu ya nyimbo za sifa na shukrani kwa Mungu. 47 Na Israeli wote, siku za Zerubabeli, na siku za Nehemia, walitoa sehemu za waimbaji na mabawabu, kama ilivyohusika kila siku; nao wakawatakasia Walawi; na Walawi wakawatakasia wana wa Haruni.

Nehemia 13

1 Siku hiyo walisoma katika kitabu cha Musa masikioni mwa watu; na ndani yake yalionekana maneno haya yameandikwa, ya kwamba Mwamoni na Mmoabi wasiingie katika kusanyiko la Mungu milele; 2 kwa sababu hawakuwalaki wana wa Israeli kwa chakula na maji, bali walimwajiri Balaamu juu yao ili awalaani; lakini Mungu aliigeuza ile laana kuwa baraka. 3 Ikawa walipoisikia torati, wakawatenga Israeli na umati wa watu waliochanganyika nao. 4 Na kabla ya hayo, Eliashibu, kuhani, aliyewekwa avisimamie vyumba vya nyumba ya Mungu wetu, kwa kuwa alikuwa karibu yake Tobia, 5 alikuwa amemtengenezea chumba kikubwa, hapo walipoweka zamani sadaka za unga, na ubani, na vyombo, na zaka za nafaka, na divai, na mafuta, walivyoamriwa kuwapa Walawi, na waimbaji, na mabawabu; tena sadaka za kuinuliwa zilizokuwa za makuhani. 6 Lakini wakati huo wote mimi sikuwako huko Yerusalemu; maana katika mwaka wa thelathini na mbili wa Artashasta, mfalme wa Babeli, nalimrudia mfalme; na baada ya siku kadha wa kadha nikaomba ruhusa tena kwa mfalme. 7 Nami nikaja Yerusalemu, nikafahamu yale mabaya, ambayo Eliashibu ameyatenda kwa ajili ya Tobia, kwa kumtengenezea chumba katika nyua za nyumba ya Mungu. 8 Nami nikasikitika sana; basi nikavitupa nje vyombo vyote vya Tobia vitoke humo chumbani. 9 Kisha nikatoa amri, nao wakavisafisha vyumba; nami nikavirudisha humo vyombo vya nyumba ya Mungu, pamoja na sadaka za unga na ubani. 10 Tena nikaona ya kwamba Walawi hawakupewa sehemu zao; basi wamekimbia Walawi na waimbaji, waliofanya kazi, kila mtu shambani kwake. 11 Ndipo nikagombana na mashehe, nikasema, Mbona nyumba ya Mungu imeachwa? Kisha nikawakusanya, nikawaweka mahali pao. 12 Ndipo Yuda wote walipoleta zaka za nafaka, na mvinyo, na mafuta, kwenye hazina. 13 Nami nikawaweka watunza hazina juu ya hazina, yaani, Shelemia kuhani, na Sadoki mwandishi, na wa Walawi, Pedaya; na wa pili wao alikuwa Hanani, mwana wa Zakuri, mwana wa Matania; kwani walihesabiwa kuwa waaminifu, na ilikuwa juu yao kuwagawia ndugu zao. 14 Unikumbukie hayo, Ee Mungu wangu, wala usifute fadhili zangu nilizozitenda kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu, na kwa taratibu zake. 15 Siku hizo naliona katika Yuda watu wengine waliokanyaga mashinikizo ya mvinyo siku ya sabato, na wengine waliochukua miganda, na kuwapakia punda zao; tena na mvinyo, na zabibu, na tini, na namna zote za mizigo, waliyoileta Yerusalemu, siku ya sabato; nami nikashuhudia juu yao siku ile waliyouza vyakula. 16 Tena wakakaa humo watu wa Tiro, walioleta samaki, na biashara za kila namna, wakawauzia wana wa Yuda siku ya sabato, na mumo humo Yerusalemu. 17 Ndipo nikagombana na wakuu wa Yuda, nikawaambia, Ni neno baya gani hili mnalofanya ninyi, na kuinajisi siku ya sabato? 18 Je! Sivyo hivyo walivyofanya baba zenu; na Mungu wetu, je! Hakuyaleta mabaya haya yote juu yetu, na juu ya mji huu? Nanyi hata hivyo mwazidi kuleta ghadhabu juu ya Israeli kwa kuinajisi sabato! 19 Ikawa malango ya Yerusalemu yalipoanza kuwa na giza kabla ya sabato, naliamuru milango ifungwe, nikaamuru isifunguliwe hata sabato iishe; na baadhi ya watumishi wangu nikawaweka juu ya malango, ili usiingizwe mzigo wo wote siku ya sabato. 20 Basi wenye biashara na wachuuzi wa bidhaa za kila namna wakalala nje ya Yerusalemu mara mbili tatu. 21 Ndipo nikawashuhudia, nikawaambia, Mbona mwalala mbele ya ukuta? Mkitenda hivi tena, nitawakamata. Tangu wakati ule hawakuja tena siku ya sabato. 22 Kisha nikawaamuru Walawi wajitakase, nao waje kuyalinda malango, ili kuitakasa siku ya sabato. Unikumbukie hayo nayo, Ee Mungu wangu, ukaniachilie sawasawa na wingi wa rehema zako. 23 Tena siku zizo hizo nikawaona wale Wayahudi waliokuwa wameoa wanawake wa Ashdodi, na Amoni, na Moabu; 24 na watoto wao wakanena nusu kwa lugha ya Ashdodi, wala hawakuweza kunena kwa Kiyahudi, bali kwa lugha ya watu hao mojawapo. 25 Nikagombana nao, nikawalaani, nikawapiga baadhi yao, na kuwang'oa nywele zao; nikawaapisha kwa Mungu, nikasema, Msiwaoze wana wao binti zenu, wala msiwatwae binti zao ili waolewe na wana wenu, wala na ninyi wenyewe. 26 Je! Sulemani, mwana wa Daudi, hakufanya dhambi kwa kutenda hayo? Lakini katika mataifa mengi hapakuwa na mfalme mwingine mfano wake. Tena alipendwa na Mungu wake, naye Mungu akamfanya mfalme juu ya Israeli; walakini wanawake wageni walimkosesha hata yeye. 27 Basi, na sisi, je! Tuwasikilize ninyi kutenda neno hili baya, hata kumhalifu Mungu wetu kwa kuwaoa wanawake wageni? 28 Na mwana mmoja wa Yoyada, mwana wa Eliashibu, kuhani mkuu, alikuwa mkwewe Sanbalati, Mhoroni, basi nikamfukuza kwangu. 29 Uwakumbuke, Ee Mungu wangu, jinsi walivyounajisi ukuhani, na agano la ukuhani na la Walawi. 30 Hivyo nikawatakasa na kila kitu kigeni, nami nikawaagizia zamu makuhani na Walawi, kila mtu kazini mwake; 31 na matoleo ya kuni nyakati zilizoamriwa, na malimbuko. Nikumbuke, Ee Mungu wangu, ili unitendee mema.

Esta 1

1 Zamani za Ahasuero; naye huyu Ahasuero alimiliki toka Bara Hindi mpaka Kushi, juu ya majimbo mia na ishirini na saba; 2 siku zile mfalme Ahasuero alipoketi katika kiti cha enzi cha ufalme wake, huko Shushani ngomeni; 3 mwaka wa tatu wa kumiliki kwake, ikawa aliwafanyia karamu maakida wake wote na majumbe wake; wakuu wa Uajemi na Umedi, watu wenye cheo na maakida wa majimbo, wakihudhuria mbele zake. 4 Akawaonyesha utajiri wa ufalme wake mtukufu, na heshima ya enzi yake bora siku nyingi, maana siku mia na themanini. 5 Hata siku hizo zilipotimia, mfalme akawafanyia karamu watu wote waliokuwapo huko Shushani ngomeni, wakubwa kwa wadogo, muda wa siku saba, katika behewa la bustani ya ngome ya mfalme. 6 Palikuwa na mapazia ya bafta, nyeupe na samawi, yamefungiwa kamba za kitani safi za rangi ya zambarau kwa pete za fedha na nguzo za marumaru; pia na vitanda vilikuwa vya dhahabu na fedha juu ya sakafu ya marumaru, mawe mekundu, na meupe, na ya manjano, na meusi. 7 Wakawanywesha kileo katika vyombo vya dhahabu, na vile vyombo vilikuwa mbalimbali, na divai tele ya namna ya kifalme, sawasawa na ukarimu wa mfalme; 8 kunywa kulikuwa kama ilivyoamriwa, bila sharti; maana ndivyo mfalme alivyowaagiza watumishi-wa-nyumbani, kila mtu afanye apendavyo. 9 Tena Vashti, malkia, naye akawafanyia karamu wanawake ndani ya nyumba ya kifalme ya mfalme Ahasuero. 10 Hata siku ya saba, mfalme alipofurahiwa moyo wake kwa divai, aliwaamuru Mehumani, Biztha, Harbona, Bigtha, Abagtha, Zethari, na Karkasi, wale wasimamizi-wa-nyumba saba waliohudumu mbele za mfalme Ahasuero, 11 wamlete Vashti, malkia, mbele ya mfalme, amevaa taji ya kifalme; ili kuwaonyesha watu na maakida uzuri wake, maana alikuwa mzuri wa uso. 12 Bali Vashti, malkia, alikataa kuja kwa amri ya mfalme kwa mkono wa wasimamizi-wa-nyumba; kwa hiyo mfalme akaghadhibika sana, na hasira yake ikawaka ndani yake. 13 Basi mfalme akawaambia wenye hekima, walio na elimu ya nyakati; maana ndivyo ilivyokuwa desturi ya mfalme kwa wote waliojua sheria na hukumu; 14 na karibu naye wameketi Karshena, Shethari, Admatha, Tarshishi, Meresi, Marsena, na Memukani, wale maakida saba wa Uajemi na Umedi, waliouona uso wa mfalme, na kuketi wa kwanza katika ufalme; akawauliza, 15 Tumfanyieje Vashti, malkia, kwa sheria, kwa sababu hakufanya kama vile alivyoamriwa na mfalme Ahasuero kwa mkono wa wasimamizi-wa-nyumba? 16 Basi Memukani akajibu mbele ya mfalme na maakida, Huyu Vashti, malkia, hakumkosa mfalme tu peke yake, ila na maakida wote, na watu wote pia walioko katika majimbo yote ya mfalme Ahasuero. 17 Kwa maana tendo hilo la malkia litajulikana na wanawake wote, hata waume zao watadharauliwa machoni pao, itakaponenwa ya kuwa mfalme Ahasuero aliamuru Vashti, malkia, aletwe mbele yake, bali hakuja. 18 Hata na leo hivi mabibi wastahiki wa Uajemi na Umedi waliokwisha kuzisikia habari za tendo lake malkia watawaambia vivi hivi maakida wote wa mfalme. Hivyo kutatokea dharau nyingi na ghadhabu tele. 19 Basi mfalme akiona vema, na itoke kwake amri ya kifalme, nayo iandikwe katika sheria za Waajemi na Wamedi isitanguke, ya kwamba Vashti asifike tena mbele ya mfalme Ahasuero; na umalkia wake mfalme ampe mwingine aliye mwema kuliko yeye. 20 Basi mbiu ya mfalme atakayoipiga itakapotangazwa katika ufalme wake wote, nao ni mkubwa, wake wote watawaheshimu waume zao, wakubwa kwa wadogo. 21 Basi neno hili likawapendeza mfalme na maakida; naye mfalme akafanya sawasawa na neno lake Memukani. 22 Kwa maana alipeleka nyaraka katika majimbo yote ya mfalme, kila jimbo kwa mwandiko wake, na kila taifa kwa lugha yake, ya kwamba kila mwanamume atawale nyumbani mwake, na kuitangaza habari hii kwa lugha ya watu wake.

Esta 2

1 Baada ya hayo, hasira yake mfalme Ahasuero ilipotulia, alimkumbuka Vashti, na vile alivyotenda, na yale yaliyoamriwa juu yake. 2 Basi watumishi wa mfalme waliomhudumu walimwambia, Mfalme na atafutiwe mabikira vijana wazuri; 3 naye mfalme aweke wasimamizi katika majimbo yote ya ufalme wake, ili wakusanye pamoja mabikira vijana wazuri wote waende Shushani ngomeni, kwenye nyumba ya wanawake mikononi mwa Hegai, msimamizi-wa-nyumba wa mfalme, mwenye kuwalinda wanawake; tena wapewe vifaa vya utakaso. 4 Naye yule msichana atakayempendeza mfalme na awe malkia badala ya Vashti. Neno hilo likampendeza mfalme, naye akafanya hivyo. 5 Basi palikuwa na Myahudi mmoja huko Shushani ngomeni; jina lake Mordekai, bin Yairi, bin Shimei, bin Kishi, wa kabila ya Benyamini; 6 ambaye kwamba amechukuliwa mateka kutoka Yerusalemu miongoni mwa wafungwa waliochukuliwa pamoja na Yekonia, mfalme wa Yuda; ambaye Nebukadreza, mfalme wa Babeli,alimchukua. 7 Naye alikuwa amemlea Hadasa, yaani, Esta, binti wa mjomba wake, kwa kuwa hana baba wala mama. Naye msichana huyu alikuwa wa umbo mzuri na uso mwema; nao walipokufa baba yake na mama yake, yule Mordekai alimtwaa kuwa binti yake yeye. 8 Basi ikawa, wakati iliposikiwa amri ya mfalme na mbiu yake, wasichana wengi wakakusanyika huko Shushani ngomeni mikononi mwa Hegai; Esta naye aliingizwa katika nyumba ya mfalme, mikononi mwa Hegai mwenye kuwalinda wanawake. 9 Yule mwanamwali akampendeza, akapokea fadhili kwake; naye akampa upesi vifaa vya utakaso, pamoja na posho zake, na vijakazi saba walio haki yake, wa nyumbani mwa mfalme. Pia akamhamisha yeye na vijakazi wake akawaweka mahali pazuri katika nyumba ya wanawake. 10 Walakini Esta hakudhihirisha kabila yake wala jamaa yake, kwa maana ndivyo alivyomwagiza Mordekai asiwadhihirishe. 11 Na yule Mordekai akawa akitembea kila siku mbele ya ua wa nyumba ya wanawake, ili ajue hali yake Esta, na hayo yatakayompata. 12 Basi ilipowadia zamu yake mwanamwali mmojawapo aingie kwa mfalme Ahasuero, hali akiisha kufanyiwa sawasawa na sheria ya wanawake miezi kumi na miwili; yaani, ndivyo zilivyotimia siku zao za utakaso, miezi sita kwa mafuta ya manemane, na miezi sita kwa manukato na vifaa vya utakaso wa wanawake; 13 mwanamwali huingia hivyo kwa mfalme; kila akitakacho hupewa kwenda nacho kutoka katika nyumba ya wanawake ili kuingia katika nyumba ya mfalme. 14 Huenda jioni, na asubuhi hurudi nyumba ya pili ya wanawake, mikononi mwa Shaashgazi, msimamizi wake mfalme, mwenye kuwalinda masuria. Wala haingii tena kwa mfalme, isipokuwa amempendeza mfalme, naye akaitwa kwa jina. 15 Hata ilipowadia zamu yake Esta, binti Abihaili, mjomba wake Mordekai, ambaye alimtwaa kuwa binti yake, ili aingie kwa mfalme, yeye hakutaka kitu, ila vile vilivyoagizwa na Hegai, msimamizi wake mfalme, mwenye kuwalinda wanawake. Naye huyu Esta alikuwa amepata kibali machoni pa wote waliomwona. 16 Basi Esta alipelekwa kwa mfalme Ahasuero, katika nyumba ya kifalme, mwezi wa kumi, ndio mwezi wa Tebethi, mwaka wa saba wa kumiliki kwake. 17 Mfalme akampenda Esta kuliko wanawake wote, naye akapata neema na kibali machoni pake kuliko mabikira wote; basi akamtia taji ya kifalme kichwani pake, akamfanya awe malkia badala ya Vashti. 18 Ndipo mfalme alipowafanyia karamu kubwa maakida wake wote na watumishi wake, yaani, karamu yake Esta; akafanya msamaha katika majimbo yote, akatoa zawadi sawasawa na ukarimu wa mfalme. 19 Basi mabikira walipokusanyika mara ya pili, Mordekai alikuwa akiketi mlangoni pa mfalme. 20 Esta alikuwa hajadhihirisha jamaa yake wala kabila yake, kama vile Mordekai alivyomwagiza; kwa maana Esta alikuwa akiyashika maagizo ya Mordekai, vile vile kama wakati alipolelewa naye. 21 Ikawa siku zile, Mordekai alipokuwa akiketi mlangoni pa mfalme, wawili katika wasimamizi wake mfalme, Bigthana na Tereshi, wangoje mlango, walighadhibika, wakataka kumpelekea mikono mfalme Ahasuero. 22 Basi Mordekai akapata kulijua jambo hilo, naye akamjulisha Esta, malkia; naye Esta akamwambia mfalme habari hiyo kwa jina la Mordekai. 23 Na jambo hilo lilipochunguzwa, na hakika ikapatikana, hao wote wawili wakatundikwa juu ya mti. Hayo pia yakaandikwa katika kitabu cha taarifa mbele ya mfalme.

Esta 3

1 Baada ya hayo mfalme Ahasuero alimwongezea cheo Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, akampandisha, akamwekea kiti chake juu ya maakida wote waliokuwapo pamoja naye. 2 Nao watumishi wote wa mfalme, walioketi mlangoni pa mfalme, wakainama na kumsujudia Hamani, maana ndivyo alivyoamuru mfalme kwa habari zake. Bali Mordekai hakuinama, wala kumsujudia. 3 Basi watumishi wa mfalme walioketi mlangoni pa mfalme wakamwambia Mordekai, Mbona wewe waihalifu amri ya mfalme? 4 Ikawa, waliposema naye kila siku asiwasikilize, wakamwarifu Hamani, ili kuona kama mambo yake Mordekai yatasimama; maana alikuwa amewaambia ya kuwa yeye ni Myahudi. 5 Hata Hamani alipoona ya kwamba Mordekai hainami wala kumsujudia, alighadhibika sana. 6 Akaona si shani kumtia mikono Mordekai peke yake; maana wamemjulisha kabila yake Mordekai; kwa hiyo Hamani alitaka kuwaangamiza Wayahudi wote waliokuwa wakikaa katika ufalme wote mzima wa Ahasuero, yaani, watu wake Mordekai. 7 Basi mwezi wa kwanza, ndio mwezi wa Nisani, mwaka wa kumi na mbili wa mfalme Ahasuero, wakapiga Puri, yaani kura, mbele yake Hamani; siku kwa siku, na mwezi kwa mwezi, hata mwezi wa kumi na mbili, ndio mwezi wa Adari. 8 Basi Hamani akamwambia mfalme Ahasuero, Kuna taifa moja waliotawanyika na kukaa mahali mahali katikati ya mataifa walioko katika majimbo yote ya ufalme wako. Nao sheria zao zimefarakana na sheria za kila taifa; wala hawazishiki amri za mfalme; kwa hiyo haimpasi mfalme kuchukuliana nao. 9 Basi, mfalme akiona vema, na iandikwe kwamba waangamizwe; nami nitalipa talanta kumi elfu za fedha mikononi mwao watakaosimamia shughuli hiyo, waziweke katika hazina ya mfalme. 10 Ndipo mfalme alipoivua pete yake mkononi, akampa Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi. 11 Kisha mfalme akamwambia Hamani, Hiyo fedha umepewa, na watu pia, fanya uonavyo vema. 12 Basi, waandishi wa mfalme wakaitwa, siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kwanza; na barua zikaandikwa, kama vile Hamani alivyoagiza vyote, kwa maakida wa mfalme, na maliwali waliokuwa juu ya kila jimbo, na wakuu wa kila taifa; kila jimbo kwa mwandiko wake, na kila taifa kwa lugha yake; zikaandikwa kwa jinsi la mfalme Ahasuero, na kutiwa muhuri kwa pete yake. 13 Barua zikapelekwa kwa mikono ya matarishi mpaka majimbo yote ya mfalme kuwaangamiza Wayahudi wote, na kuwaua, na kuwafisha, vijana kwa wazee, watoto wachanga na wanawake pia, siku moja, yaani, siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili ndio mwezi wa Adari; na kuyachukua mali yao kuwa nyara. 14 Nakili ya andiko, ya kupigwa mbiu katika kila jimbo, ilitangazwa kwa mataifa yote wawe tayari siku ile ile. 15 Matarishi wakaondoka wakaenda haraka kwa amri ya mfalme; kukapigwa mbiu huko Shushani ngomeni. Mfalme na Hamani wakaketi ili kunywa divai; bali mji wa Shushani ukafadhaika.

Esta 4

1 Basi Mordeikai alipojua mambo yote yaliyofanyika, alizirarua nguo zake, akajivika gunia pamoja na majivu, akatoka hata kufika katikati ya mji, akalia kwa sauti kuu ya uchungu. 2 Pia akafika hata mbele ya mlango wa mfalme; maana hakuna awezaye kuingia ndani ya mlango wa mfalme hali amevaa magunia. 3 Na katika kila jimbo, ambako amri ya mfalme na mbiu yake imewasili, palikuwako msiba mkuu kwa Wayahudi, na kufunga, na kulia, na kuomboleza; hata na wengi wakalala juu ya gunia na majivu. 4 Basi wajakazi wake Esta, na wasimamizi wake wa nyumba, wakamjia, wakampasha habari; naye malkia akahuzunika mno; akampelekea Mordekai mavazi, ili kumvika, na kumwondolea gunia lake; walakini yeye asikubali. 5 Kisha Esta akamwita Hathaki, msimamizi-wa-nyumba mmojawapo wa mfalme, aliyemwagiza amhudumu Esta, akamtuma kwa Mordekai, ili ajue mambo hayo, na maana yake ni nini. 6 Basi yule Hathaki akatoka nje kumwendea Mordekai kwenye uwanda wa mji ulipo mbele ya mlango wa mfalme. 7 Naye Mordekai akamweleza yote yaliyompata, na hesabu ya fedha Hamani aliyoahidi kulipa katika hazina ya mfalme, ili Wayahudi waangamizwe. 8 Pia akampa na nakili ya andiko la mbiu ya kuwaangamiza, iliyotangazwa Shushani, ili amwonyeshe Esta, na kumweleza; tena amwagize aingie kwa mfalme, kumsihi na kuwaombea watu wake. 9 Basi Hathaki akaja, akamwambia Esta maneno ya Mordekai. 10 Ndipo Esta akasema na Hathaki, akamtuma tena kwa Mordekai, kusema, 11 Watumwa wote wa mfalme wanajua sana, hata na watu wa majimbo ya mfalme, ya kwamba mtu ye yote, akiwa mwanamume au mwanamke, atakayemjia mfalme katika ua wa ndani, wala hakuitwa, kuna sheria moja kwake, ni kwamba auawe; isipokuwa yeye ambaye mfalme atamnyoshea fimbo ya dhahabu, ili aishi; wala mimi sikuitwa niingie kwa mfalme yapata siku thelathini. 12 Basi wakamwambia Mordekai maneno ya Esta. 13 Naye Mordekai akawaagiza wampelekee Esta jibu la kusema, Wewe usijidhanie kuwa wewe utaokoka nyumbani mwa mfalme, zaidi ya Wayahudi wote. 14 Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine; ila wewe utaangamia pamoja na mlango wote wa baba yako; walakini ni nani ajuaye kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huo? 15 Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai, 16 Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie. 17 Basi Mordekai akaenda zake, akafanya yote kama vile Esta alivyomwagiza.

Esta 5

1 Ikawa siku ya tatu Esta alijivika mavazi yake ya kifalme, akasimama katika ua wa ndani wa nyumba ya mfalme, kuielekea nyumba ya mfalme; naye mfalme akaketi juu ya kiti chake cha enzi katika nyumba ya mfalme, kuuelekea mlango wa nyumba. 2 Ikawa, mfalme alipomwona malkia Esta amesimama uani, yeye akapata kibali machoni pake; naye mfalme akamnyoshea Esta fimbo ya dhahabu aliyokuwa nayo mkononi. Basi Esta akakaribia, akaigusa ncha ya fimbo. 3 Mfalme akamwambia, Malkia Esta, wataka nini? Nayo ni haja gani uliyo nayo? Utapewa hata nusu ya ufalme. 4 Esta akasema, Mfalme akiona vema, na aje leo, mfalme na Hamani, kwenye karamu niliyomwandalia. 5 Basi mfalme akasema, Mhimize Hamani, ili ifanyike kama Esta alivyosema. Hivyo mfalme na Hamani wakafika katika karamu ile aliyoiandaa Esta. 6 Basi mfalme akamwambia Esta pale penye karamu ya divai, Dua yako ni nini? Nawe utapewa; na haja yako ni nini? Hata nusu ya ufalme utafanyiziwa. 7 Esta akajibu, na kusema, Dua yangu ni hii, na haja yangu ni hii, 8 Ikiwa nimepata kibali machoni pa mfalme, na mfalme akiona vema kunipa niombalo, na kunifanyizia haja yangu, na aje tena mfalme na Hamani kwenye karamu nitakayowaandalia, nami kesho nitafanya kama vile mfalme alivyosema. 9 Basi Hamani alitoka siku ile kwa furaha na ukunjufu wa moyo; lakini Hamani alipomwona Mordekai mlangoni pa mfalme, ya kwamba hasimami wala kutetemeka mbele yake, alijaa ghadhabu juu ya Mordekai. 10 Walakini Hamani akajizuia, akaenda zake nyumbani kwake; akatuma kuwaita rafiki zake na Zereshi mkewe. 11 Naye Hamani akawasimulia habari za fahari ya mali zake, na wingi wa watoto wake, nayo mambo yote pia ambayo mfalme amemfanikisha katika hayo, na jinsi alivyompandisha juu ya maakida na watumishi wa mfalme. 12 Zaidi ya hayo Hamani akasema, Naye malkia Esta hakumkaribisha mtu ye yote pamoja na mfalme katika karamu aliyoiandaa, ila mimi peke yangu; hata na kesho pia nimealikwa naye pamoja na mfalme. 13 Bali haya yote yanifaa nini, pindi nimwonapo yule Mordekai, Myahudi, ameketi mlangoni pa mfalme? 14 Basi Zereshi mkewe akamwambia, na rafiki zake wote, Na ufanyizwe mti wa mikono hamsini urefu wake, na kesho asubuhi useme na mfalme ili Mordekai atundikwe juu yake; ndipo utakapoingia kwa kicheko pamoja na mfalme karamuni. Basi neno likampendeza Hamani, akaufanyiza ule mti.

Esta 6

1 Usiku ule mfalme hakupata usingizi; akaamuru aletewe kitabu cha maandiko ya taarifa, nayo yakasomwa mbele ya mfalme. 2 Ikaonekana kuwa imeandikwa ya kwamba Mordekai aliwachongea Bigthana na Tereshi, wasimamizi wawili wa mfalme, katika hao waliolinda mlango, waliotaka kumtia mikono mfalme Ahasuero. 3 Mfalme akasema, Je! Ni heshima gani au jaha gani Mordekai aliyofanyiziwa kwa ajili ya hayo? Watumwa wa mfalme waliomhudumu wakamwambia, Hakuna alilofanyiziwa. 4 Mfalme akasema, Yupo nani behewani? Ikawa Hamani alikuwa ameingia katika ua wa nje wa nyumba ya mfalme, aseme na mfalme, ili kumtundika Mordekai juu ya mti ule aliomwekea tayari. 5 Basi watumwa wa mfalme wakamwambia, Tazama, Hamani yupo, amesimama behewani. Mfalme akasema, Na aingie. 6 Basi Hamani akaingia. Mfalme akamwambia, Afanyiziwe nini yule ambaye mfalme apenda kumheshimu? Hamani akasema moyoni mwake, Ni nani ambaye mfalme apenda kumheshimu kuliko mimi? 7 Basi Hamani akamwambia mfalme, Yule ambaye mfalme apenda kumheshimu, 8 na aletewe mavazi ya kifalme ambayo mfalme amezoea kuyavaa, na farasi ambaye mfalme humpanda mwenyewe, ambaye ametiwa taji ya kifalme kichwani; 9 na yale mavazi na yule farasi akabidhiwe mkononi mmojawapo wa maakida wa mfalme aliye mstahiki; ili makusudi amvike yule ambaye mfalme apenda kumheshimu, na kumrakibisha juu ya farasi kuipitia njia kuu ya mjini, na kupiga mbiu mbele yake, kusema, Hivyo ndivyo atakavyofanyiziwa mtu yule ambaye mfalme apenda kumheshimu. 10 Basi mfalme akamwambia Hamani, Hima! Twaa mavazi na farasi kama ulivyosema, ukamfanyizie vivyo hivyo Mordekai, Myahudi, aketiye mlangoni pa mfalme; lisipungue neno lo lote katika yote uliyoyasema. 11 Ndipo Hamani alipoyatwaa mavazi na farasi, akamvika Mordekai yale mavazi, akamrakibisha juu ya farasi kuipitia njia kuu ya mjini, akapiga mbiu mbele yake, Hivyo ndivyo atakavyofanyiziwa mtu yule ambaye mfalme apenda kumheshimu. 12 Kisha Mordekai akarudi kwenye mlango wa mfalme. Bali Hamani akaenda mbio nyumbani kwake, mwenye msiba, na kichwa chake kimefunikwa. 13 Basi Hamani akawasimulia Zereshi mkewe na rafiki zake wote kila neno lililompata. Kisha watu wake wenye hekima na Zereshi mkewe wakamwambia, Ikiwa huyu Mordekai, ambaye umeanza kuanguka mbele yake, ni wa uzao wa Wayahudi, wewe hutamweza, bali kuanguka utaanguka mbele yake. 14 Hata walipokuwa katika kusema naye, wasimamizi-wa-nyumba wa mfalme walifika, wakahimiza kumleta Hamani katika karamu ile aliyoiandaa Esta.

Esta 7

1 Basi mfalme na Hamani walikuja kula karamu pamoja na malkia Esta. 2 Mfalme akamwambia Esta tena siku ya pili pale pale penye karamu ya divai, Malkia Esta, dua yako ni nini? Nawe utapewa; na haja yako ni nini? Hata nusu ya ufalme utafanyiziwa. 3 Ndipo malkia Esta alipojibu, akasema, Mfalme, ikiwa nimepata kibali machoni pako, na mfalme akiona vema, nipewe maisha yangu kuwa dua yangu, na watu wangu kuwa haja yangu. 4 Maana tumeuzwa, mimi na watu wangu, ili tuharibiwe, na kuuawa, na kuangamia. Kama tungaliuzwa kuwa watumwa na wajakazi, ningalinyamaza; ila hata hivyo msiba wetu haulinganishwi na hasara ya mfalme. 5 Ndipo mfalme Ahasuero aliponena, akamwambia malkia Esta, Ni nani huyu, tena yuko wapi, ambaye moyoni mwake alithubutu kufanya hivi? 6 Esta akasema, Ni mtesi, tena ni adui, ndiye huyu Hamani, mtu mbaya kabisa. Mara Hamani akaingiwa na hofu mbele ya mfalme na malkia. 7 Mfalme akaondoka katika ghadhabu yake kutoka kwenye karamu ya divai, akaingia bustani ya ngome. Hamani naye akasimama ili ajitakie maisha yake kwa malkia Esta; kwa kuwa aliona ya kwamba amekusudiwa madhara na mfalme. 8 Kisha mfalme akarudi kutoka katika bustani ya ngome hata mahali pa karamu ya divai. Ikawa Hamani amejitupa chini penye kitanda alipokuwapo Esta. Mfalme akasema, Namna gani! Je! Atamfanyia malkia jeuri hata machoni pangu nyumbani mwangu? Na neno lilipotoka kinywani mwa mfalme, wakamfunika uso Hamani. 9 Ndipo aliposema Harbona, msimamizi-wa-nyumba mmojawapo wa wale waliohudhuria mbele ya mfalme, Tazama, basi, mti wa mikono hamsini urefu wake, Hamani aliomwekea tayari Mordekai, ambaye alinena vema kwa ajili ya mfalme, upo umesimamishwa nyumbani kwa Hamani. Mfalme akasema, Mtundikeni juu yake. 10 Basi wakamtundika Hamani juu ya mti aliomwekea tayari Mordekai. Ghadhabu ya mfalme ikatulia.

Esta 8

1 Siku ile mfalme Ahasuero alimpa malkia Esta nyumba yake Hamani, yule adui ya Wayahudi. Mordekai naye akahudhuria mbele ya mfalme; kwa maana Esta alikuwa amedhihirisha alivyomhusu. 2 Basi mfalme akaivua pete yake, aliyompokonya Hamani, akampa Mordekai. Naye Esta akamweka Mordekai kuwa juu ya mlango wake Hamani. 3 Tena Esta akasema na mfalme mara ya pili, akaanguka miguuni pake, akamsihi kwa machozi ayaondoe madhara ya Hamani, Mwagagi, na shauri alilowafanyia Wayahudi. 4 Ndipo mfalme alipomnyoshea Esta fimbo yake ya dhahabu. Basi Esta akaondoka, akasimama mbele ya mfalme. 5 Akasema, Mfalme akiona vema, nami nikiwa nimepata kibali machoni pake, na neno likionekana jema mbele ya mfalme, nami nikimpendeza machoni pake, iandikwe kuzitangua barua za Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, alizotunga na kuziandika ili kuwaangamiza Wayahudi walioko katika majimbo yote ya mfalme. 6 Kwa maana niwezeje kuyaona mabaya yatakayowajia watu wangu? Au niwezeje kuyatazama maangamizo ya jamaa zangu? 7 Mfalme Ahasuero akawaambia malkia Esta na Mordekai, Myahudi, kusema, Tazama, nimekwisha kumpa Esta nyumba yake Hamani, naye mwenyewe wamekwisha kumtundika juu ya mti, kwa sababu aliwatia mikono Wayahudi. 8 Basi waandikieni Wayahudi pia vyo vyote mpendavyo, kwa jina la mfalme, mkatie muhuri kwa pete ya mfalme; kwa kuwa andiko lililoandikwa kwa jina la mfalme na kutiwa muhuri kwa pete ya mfalme hakuna awezaye kulitangua. 9 Basi, waandishi wa mfalme wakaitwa pale pale, siku ya ishirini na tatu ya mwezi wa tatu, ndio mwezi wa Siwani; na kama vile Mordekai alivyoamuru, Wayahudi wakaandikiwa, pamoja na maakida na maliwali, na wakuu wa majimbo toka Bara Hindi mpaka Kushi, majimbo mia na ishirini na saba, kila jimbo kwa mwandiko wake, na kila taifa kwa lugha yake; na Wayahudi kwa mwandiko wao na kwa lugha yao. 10 Akaandika kwa jina la mfalme Ahasuero, na kutia muhuri kwa pete ya mfalme, akazipeleka barua kwa matarishi, wamepanda farasi, wamepanda wanyama wepesi sana waliotumika kwa huduma ya mfalme, ndio waliozalishwa katika zizi la mfalme. 11 Katika barua hizo mfalme aliwaruhusu Wayahudi wakusanyike katika kila mji na kuzisimamia maisha zao, kuangamiza, na kuua, na kulifisha jeshi lote la watu na la jimbo watakaowaondokea, wao na wadogo wao na wanawake; na kuyachukua mali yao kuwa nyara; 12 siku moja, katika majimbo yote ya mfalme Ahasuero, yaani, siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili, ndio mwezi wa Adari. 13 Nakili ya andiko, ya kupigwa mbiu katika kila jimbo, ilitangazwa kwa mataifa yote, na kwa Wayahudi, wawe tayari siku ile ile kujilipiza kisasi juu ya adui zao. 14 Matarishi wakaondoka, wamepanda wanyama wepesi sana waliotumika kwa huduma ya mfalme, huku wakihimizwa na kusukumizwa kwa amri ya mfalme; kukapigwa mbiu huko Shushani ngomeni. 15 Naye Mordekai akatoka usoni pa mfalme, amevaa mavazi ya kifalme, ya rangi ya samawi na nyeupe, mwenye taji kubwa ya dhahabu, na joho ya kitani safi na rangi ya zambarau. Mji wa Shushani wakapaza sauti, wakashangilia. 16 Ikawa nuru na furaha na shangwe na heshima kwa Wayahudi. 17 Na katika kila jimbo, na kila mji, po pote palipowasili amri ya mfalme na mbiu yake, Wayahudi wakapata furaha na shangwe, karamu na sikukuu. Hata wengi wa watu wa nchi wakajifanya Wayahudi, kwa kuwa hofu ya Wayahudi imewaangukia.

Esta 9

1 Hata ulipofika mwezi wa kumi na mbili, ndio mwezi wa Adari, siku yake ya kumi na tatu, amri ya mfalme na mbiu yake ilipowadia kutekelezwa; ambayo siku ile adui za Wayahudi walitumaini kuwatawala, bali kumebadilika kinyume, hata Wayahudi waliwatawala wale waliowachukia; 2 siku ile ile Wayahudi wakakusanyika mijini mwao katika majimbo yote ya mfalme Ahasuero ili kuwatia mikono wale watu waliowatakia hasara; wala asiweze mtu kuwazuia, kwa kuwa hofu yao imewaangukia watu wote. 3 Nao maakida wa majimbo, na majumbe, na maliwali, na wale waliofanya shughuli ya mfalme, waliwasaidia Wayahudi; kwa sababu hofu ya Mordekai imewaangukia. 4 Maana Mordekai alikuwa mkuu nyumbani mwa mfalme, na sifa yake imevuma katika majimbo yote, kwa kuwa huyo Mordekai amezidi kukuzwa. 5 Basi Wayahudi wakawapiga adui zao wote mapigo ya upanga, na machinjo, na maangamizo, wakawatenda kama wapendavyo wale waliowachukia. 6 Hata huko Shushani ngomeni Wayahudi wakawaua watu mia tano, na kuwaangamiza. 7 Wakawaua na Parshandatha, na Dalfoni, na Aspatha, 8 na Poratha, na Adalia, na Aridatha, 9 na Parmashta, na Arisai, na Aridai, na Waizatha, 10 wana kumi wa Hamani bin Hamedatha, adui ya Wayahudi; walakini juu ya nyara hawakuweka mikono. 11 Siku ile mfalme akaletewa hesabu ya hao waliouawa huko Shushani ngomeni. 12 Mfalme akamwambia malkia Esta, Wayahudi wamewaua watu mia tano hapa Shushani ngomeni na kuwaangamiza, pamoja na wana kumi wa Hamani, je! Wamefanyaje basi katika majimbo ya mfalme yaliyosalia! Basi, una nini uombalo? Nawe utapewa; ama unayo haja gani tena? Nayo itatimizwa. 13 Ndipo Esta aliposema, Mfalme akiona vema, Wayahudi walioko Shushani na wapewe ruhusa kufanya tena kesho sawasawa na mbiu ya leo, na hao wana kumi wa Hamani watundikwe juu ya mti ule. 14 Mfalme akaamuru vifanyike vivyo hivyo, mbiu ikapigwa huko Shushani, wakawatundika wale wana kumi wa Hamani. 15 Basi Wayahudi wa Shushani wakakusanyika tena siku ya kumi na nne pia ya mwezi wa Adari, wakawaua watu mia tatu huko Shushani; walakini juu ya nyara hawakuweka mikono. 16 Nao Wayahudi wengine waliokaa katika majimbo ya mfalme walikusanyika, wakazishindania maisha zao, wakajipatia raha mbele ya adui zao, wakawaua waliowachukia, watu sabini na tano elfu; walakini juu ya nyara hawakuweka mikono. 17 Hii ndiyo siku ya kumi na tatu ya mwezi wa Adari; na siku ya kumi na nne ya mwezi huo wakapumzika, wakaifanya kuwa siku ya karamu na furaha. 18 Lakini Wayahudi wa Shushani walikusanyika siku ya kumi na tatu ya mwezi huo, na siku ya kumi na nne pia; na siku ya kumi na tano ya mwezi uo huo wakapumzika, wakaifanya kuwa siku ya karamu na furaha. 19 Kwa sababu hii Wayahudi wa vijijini, wakaao katika miji isiyo na boma, huishika siku ya kumi na nne ya mwezi wa Adari, kuwa siku ya furaha na karamu, sikukuu ya kupelekeana zawadi. 20 Basi Mordekai aliyaandika mambo hayo; naye akapeleka barua kwa Wayahudi wote waliokaa katika majimbo yote ya mfalme Ahasuero, waliokuwa karibu na waliokuwa mbali, 21 kuwaonya wazishike siku ya kumi na nne ya mwezi wa Adari, na siku ya kumi na tano yake, mwaka kwa mwaka, 22 ambazo ni siku Wayahudi walipojipatia raha mbele ya adui zao, na mwezi uliogeuzwa kwao kuwa furaha badala ya huzuni, na kuwa sikukuu badala ya kilio; wazifanye siku hizo ziwe za karamu na furaha, za kupeana zawadi na za kuwapa maskini vipawa. 23 Nao Wayahudi wakakubali kufanya kama walivyoanza, na kama Mordekai alivyowaandikia; 24 kwa sababu Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi wote, alikuwa amefanya shauri juu ya Wayahudi ili kuwaangamiza, akapiga Puri, yaani kura, ili kuwakomesha na kuwaangamiza pia; 25 bali mfalme alipoarifiwa, aliamuru kwa barua ya kwamba hilo shauri baya alilolifanya juu ya Wayahudi limrudie kichwani pake mwenyewe; na ya kwamba yeye na wanawe watundikwe juu ya mti. 26 Hivyo wakaziita siku hizo Purimu, kwa jina la Puri. Basi, kwa ajili ya maneno yote ya barua hiyo, na kwa yale waliyoyaona wenyewe juu ya jambo hilo, na mambo yenyewe yaliyowajia, 27 Wayahudi wakaagiza na kutadariki juu yao wenyewe, na juu ya wazao wao, na juu ya wote watakaojiunga nao, isikome, ya kwamba watazishika siku hizo mbili sawasawa na andiko lile, na kwa majira yake kila mwaka; 28 siku hizo zikumbukwe na kushikwa kwa vizazi vyote na kila jamaa, katika kila jimbo na kila mji; wala siku hizo za Purimu zisikome katikati ya Wayahudi, wala kumbukumbu lake lisiishe kwa wazao wao. 29 Ndipo malkia Esta, binti Abihaili, pamoja na Mordekai Myahudi, alipoandika kwa mamlaka yote kuithibitisha barua hii ya pili ya Purimu. 30 Akapeleka barua kwa Wayahudi wote katika majimbo yote mia na ishirini na saba ya ufalme wake Ahasuero, maneno ya amani na kweli, 31 ili kuzithibitisha siku hizo za Purimu kwa majira yake, kama Mordekai Myahudi na malkia Esta walivyoamuru, na kama walivyojiagizia juu yao wenyewe, na juu ya wazao wao, kwa habari ya kufunga na kilio. 32 Amri yake Esta ikayathibitisha mambo hayo ya Purimu; ikaandikwa katika kitabu.

Esta 10

1 Basi mfalme Ahasuero alitoza kodi katika nchi na katika visiwa vya bahari. 2 Na matendo yake yote yenye nguvu na ya ushujaa, na habari zote za ukuu wake Mordekai ambao alipewa na mfalme, hazikuandikwa katika kitabu-cha-taarifa cha wafalme wa Umedi na Uajemi? 3 Kwa maana Mordekai Myahudi akawa wa pili wake mfalme Ahasuero, na mkuu wa Wayahudi, amependeza mbele ya jamii ya ndugu zake; ambaye aliwatafuta watu wake wema, na kuiangalia hali njema ya wazao wao wote.

Ayubu 1

1 Palikuwa na mtu katika nchi ya Usi, jina lake alikuwa akiitwa Ayubu; mtu huyo alikuwa mkamilifu na mwelekevu, ni mmoja aliyemcha Mungu, na kuepukana na uovu. 2 Kisha walizaliwa kwake wana saba, na binti watatu. 3 Mali yake nayo yalikuwa ni kondoo elfu saba, na ngamia elfu tatu, na jozi za ng'ombe mia tano, na punda wake mia tano, na watu wa nyumbani wengi sana; basi hivi mtu huyo alikuwa ni mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki. 4 Nao wanawe huenda na kufanya karamu katika nyumba ya kila mmoja wao kwa siku yake; nao wakatuma na kuwaita maumbu yao watatu ili waje kula na kunywa pamoja nao. 5 Basi ilikuwa, hapo hizo siku za karamu zao zilipokuwa zimetimia, Ayubu hutuma kwao akawatakasa, kisha akaamka asubuhi na mapema, na kusongeza sadaka za kuteketezwa kama hesabu yao wote ilivyokuwa; kwani Ayubu alisema, Yumkini kwamba hawa wanangu wamefanya dhambi, na kumkufuru Mungu mioyoni mwao. Ndivyo alivyofanya Ayubu sikuzote. 6 Ilikuwa, siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za Bwana, Shetani naye akaenda kati yao. 7 Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. 8 Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. 9 Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? 10 Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. 11 Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako. 12 Bwana akamwambia Shetani, Tazama, yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako; lakini usinyoshe mkono wako juu yake yeye mwenyewe. Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana. 13 Ilitukia siku moja hao wanawe na binti zake walipokuwa wakila na kunywa divai katika nyumba ya ndugu yao mkubwa, 14 mjumbe akamfikilia Ayubu na kumwambia, Hao ng'ombe walikuwa wakilima, na punda walikuwa wakilisha karibu nao; 15 mara Waseba wakawashambulia, wakawachukua wakaenda nao; naam, wamewaua hao watumishi kwa makali ya upanga, mimi peke yangu nimepona, mimi tu, kukuletea habari. 16 Huyo alipokuwa akali akinena, akatokea na mwingine, na kusema, Moto wa Mungu umeanguka kutoka mbinguni na kuwateketeza kondoo, na wale watumishi, na kuwaangamiza; mimi peke yangu nimepona, mimi tu, kukuletea habari. 17 Huyo alipokuwa akali akinena, akatokea na mwingine, na kusema, Wakaldayo walifanya vikosi vitatu, wakawaangukia ngamia, wakaenda nao, naam, wamewaua wale watumishi kwa makali ya upanga; mimi peke yangu nimepona, mimi tu, kukuletea habari. 18 Huyo alipokuwa akali akinena, akatokea na mwingine, na kusema, Wanao na binti zako walikuwa wakila na kunywa divai katika nyumba ya ndugu yao mkubwa; 19 mara, tazama, upepo wenye nguvu ukatoka pande za jangwani, ukaipiga hiyo nyumba pembe zake nne, nayo ikawaangukia hao vijana, nao wamekufa; na mimi peke yangu nimepona, mimi tu, kukuletea habari. 20 Ndipo Ayubu akainuka, akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake, na kuanguka chini, na kusujudia; 21 akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe. 22 Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.

Ayubu 2

1 Tena kulikuwa na siku hao wana wa Mungu walipokwenda kujihudhurisha mbele za Bwana, Shetani naye akaenda kati yao, ili kujihudhurisha mbele za Bwana. 2 Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi? Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. 3 Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu; naye hata sasa anashikamana na utimilifu wake, ujapokuwa ulinichochea juu yake, ili nimwangamize pasipokuwa na sababu. 4 Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake. 5 Lakini sasa nyosha mkono wako, uuguse mfupa wake na nyama yake, naye atakukufuru mbele za uso wako. 6 Bwana akamwambia Shetani, Tazama, yeye yumo mkononi mwako; lakini tunza tu uhai wake. 7 Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. 8 Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni. 9 Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. 10 Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake. 11 Basi ikawa hao rafikize Ayubu watatu walipopata habari ya mabaya hayo yote yaliyomfikilia, wakaja kila mtu kutoka mahali pake; nao ni Elifazi Mtemani, na Bildadi Mshuhi, na Sofari Mnaamathi; wakapatana pamoja ili waende kumlilia Ayubu na kumtuliza moyo. 12 Basi walipovua macho yao, nao wakali mbali, wasimtambue, wakainua sauti zao na kulia; kila mmoja akararua joho yake, wakarusha mavumbi juu ya vichwa vyao kuelekea mbinguni. 13 Kisha wakaketi nchi pamoja naye muda wa siku saba, mchana na usiku, wala hapana mmoja aliyenena naye neno lo lote; kwa maana waliona ya kuwa mashaka yake aliyo nayo ni makuu mno.

Ayubu 3

1 Baada ya hayo Ayubu akafunua kinywa chake, na kuilaani siku yake. 2 Ayubu akajibu, na kusema; 3 Na ipotelee mbali ile siku niliyozaliwa mimi, Na ule usiku uliosema, Mtoto mume ametungishwa mimba. 4 Siku hiyo na iwe giza; Mungu asiiangalie toka juu, Wala mwanga usiiangazie. 5 Ishikwe na giza, giza tupu, kuwa yake; Wingu na likae juu yake; Chote kiifanyacho siku kuwa giza na kiitishe. 6 Tena usiku huo, na ushikwe na giza kuu; Usihesabiwe katika siku za mwaka; Wala kutiwa katika hesabu ya miezi. 7 Tazama, usiku huo na uwe tasa; Wala isiwe ndani yake sauti ya shangwe. 8 Na waulaani hao waulaanio mchana, Hao walio tayari kumwamsha huyo lewiathani. 9 Nyota za mapambazuko yake na ziwe giza; Na utafute mwanga lakini usiupate; Wala usiyaone makope ya asubuhi; 10 Kwa sababu haukuifunga milango ya tumbo la mamangu. Wala kunifichia taabu machoni. 11 Mbona si kufa mimi tokea mimbani? Mbona nisitoe roho hapo nilipotoka tumboni? 12 Mbona hayo magoti kunipokea? Au hayo maziwa, hata nikanyonya? 13 Maana hapo ningelala na kutulia; Ningelala usingizi; na kupata kupumzika; 14 Pamoja na wafalme na washauri wa dunia, Hao waliojijengea maganjoni; 15 Au pamoja na wakuu wenye dhahabu, Waliozijaza fedha nyumba zao; 16 Au, kama kuzikwa mimba iliyoharibika, nisingekuwako; Kama wachanga wasiouona mwanga kabisa. 17 Huko waovu huacha kusumbua; Huko nako hao waliochoka wapumzika 18 Huko wafungwa waona raha pamoja; Hawaisikii sauti yake msimamizi. 19 Wakuu na wadogo wako huko; Mtumishi yu huru kwa bwana wake. 20 Mbona yeye aliye mashakani kupewa mwanga, Na hao wenye uchungu rohoni kupewa uhai; 21 Ambao wangojea mauti, lakini hawayapati; Na kuyachimbulia zaidi ya kutafuta hazina iliyostirika; 22 Ambao wafurahi mno, Na kushangilia watakapoliona kaburi? 23 Kwa nini mtu aliyezibiwa njia kupewa mwanga, Ambaye Mungu amemzingira kwa ukingo? 24 Kwani kuugua kwangu kwaja kana kwamba ni chakula, Na kunguruma kwangu kumemiminika kama maji. 25 Maana jambo hilo nichalo hunipata, Nalo linitialo hofu hunijilia. 26 Mimi sioni raha, wala situlii, wala kupumzika; Lakini huja taabu.

Ayubu 4

1 Ndipo huyo Elifazi, Mtemani, akajibu na kusema, 2 Mtu akijaribu kuzungumza nawe, je! Utaona ni vibaya? Lakini ni nani awezaye kujizuia asinene? 3 Tazama, wewe umewafunza watu wengi, Nawe umeitia nguvu mikono iliyokuwa minyonge. 4 Maneno yako yamemtegemeza huyo aliyekuwa anaanguka, Nawe umeyaimarisha magoti manyonge. 5 Lakini sasa haya yamekufikilia wewe, nawe wafa moyo; Yamekugusa, nawe wafadhaika. 6 Je! Dini yako siyo mataraja yako, Na matumaini yako si huo uelekevu wa njia zako? 7 Kumbuka, tafadhali, ni nani aliyeangamia akiwa hana hatia? Au hao waelekevu, walikatiliwa mbali wapi? 8 Kama mimi nilivyoona, hao walimao maovu, Na kupanda madhara, huvuna yayo hayo. 9 Kwa pumzi za Mungu huangamia. Na kwa kuvuma kwa hasira zake humalizika. 10 Kunguruma kwake simba, na sauti ya simba mkali, Na meno ya simba wachanga, yamevunjika. 11 Simba mzee huangamia kwa kukosa mawindo, Nao watoto wa simba mke wametawanyika mbalimbali. 12 Basi, nililetewa neno kwa siri, Sikio langu likasikia manong'ono yake. 13 Katika mawazo yaliyotoka katika maono ya usiku, Hapo usingizi mzito uwaangukiapo wanadamu. 14 Hofu iliniangukia na kutetema, Iliyoitetemesha mifupa yangu yote. 15 Ndipo pepo ilipita mbele ya uso wangu; Na nywele za mwili wangu zilisimama. 16 Hiyo pepo ilisimama kimya, nisiweze kutambua sura zake, Mfano ulikuwa mbele ya macho yangu; Kulikuwa kimya, nami nilisikia sauti, ikinena, 17 Je! Binadamu atakuwa na haki kuliko Mungu? Je! Mtu atakuwa safi kuliko Muumba wake? 18 Tazama, yeye hawategemei watumishi wake; Na malaika zake huwahesabia upuzi; 19 Je! Si zaidi sana hao wakaao katika nyumba za udongo, Ambazo misingi yao i katika mchanga, Hao waliosetwa mbele ya nondo! 20 Kati ya asubuhi na jioni huvunjwa-vunjwa; Waangamia milele wala hapana atiaye moyoni. 21 Je! Kamba ya hema yao haikung'olewa ndani yao? Wafa, kisha hali hawana akili.

Ayubu 5

1 Haya, ita sasa; je! Yuko atakayekujibu? Nawe utamwelekea yupi katika hao watakatifu? 2 Kwani hasira humwua mtu mpumbavu, Nao wivu humwua mjinga. 3 Nimewaona wapumbavu wakishusha mizizi; Lakini mara niliyalaani maskani yake. 4 Watoto wake wako mbali na wokovu, Nao wamesongwa langoni, Wala hapana atakayewaponya. 5 Mavuno yake wale wenye njaa huyala, Na kuyatwaa hata kuyatoa miibani, Nao wenye kiu huzitwetea mali zao. 6 Kwani taabu haitoki mchangani, Wala mashaka hayachipuki katika nchi; 7 Lakini mwanadamu huzaliwa ili apate mashaka, Kama cheche za moto zirukavyo juu. 8 Lakini mimi ningemtafuta Mungu, Ningemwekea Mungu daawa yangu; 9 Yeye afanyaye mambo makuu, yasiyotambulikana; Mambo ya ajabu yasiyo na hesabu; 10 Yeye atoaye mvua inyeshe juu ya nchi, Na kuyapeleka maji mashambani; 11 Awainuaye juu hao walio chini; Na hao waombolezao hukuzwa wawe salama. 12 Yeye huyatangua mashauri ya wadanganyifu, Mikono yao isipate kuyatimiza makusudi yao. 13 Yeye huwanasa wenye hekima katika hila yao wenyewe; Na mashauri ya washupavu yaharibika kwa haraka. 14 Wao hupatwa na giza wakati wa mchana, Hupapasa mchana vilevile kama usiku. 15 Lakini yeye huokoa na upanga wa kinywa chao, Hata kumwokoa mhitaji na mkono wake aliye hodari. 16 Basi hivi huyo maskini ana matumaini, Na uovu hufumba kinywa chake. 17 Tazama, yu heri mtu yule Mungu amwadhibuye; Kwa hiyo usidharau kurudiwa na huyo Mwenyezi. 18 Kwani yeye huumiza, lakini tena huuguza; Yeye hutia jeraha, na mikono yake huponya. 19 Yeye atakuokoa na mateso sita; Naam, hata katika saba hapana uovu utakaokugusa. 20 Wakati wa njaa atakukomboa na mauti; Na vitani atakukomboa na nguvu za upanga. 21 Utafichwa na mapigo ya ulimi; Wala usiogope maangamizo yatakapokuja. 22 Wewe utayacheka maangamizo na njaa; Wala hutawaogopa wanyama wakali wa nchi. 23 Kwani utakuwa na mapatano na mawe ya bara; Nao wanyama wa bara watakuwa na amani kwako. 24 Nawe utajua ya kwamba hema yako ina salama; Na zizi lako utaliaua, wala usikose kitu. 25 Tena utajua ya kwamba uzao wako utakuwa mwingi, Na vizazi vyako watakuwa kama nyasi za nchi. 26 Utafika kaburini mwenye umri mtimilifu, Kama mganda wa ngano ulivyo wakati wake. 27 Tazama, haya tumeyapeleleza, ndivyo yalivyo; Yasikie, uyajue, ili upate mema.

Ayubu 6

1 Ndipo Ayubu akajibu na kusema, 2 Laiti uchungu wangu ungepimwa, Na msiba wangu kutiwa katika mizani pamoja! 3 Kwa kuwa sasa ungekuwa mzito kuliko mchanga wa bahari; Kwa hiyo maneno yangu yamekuwa ya haraka. 4 Kwa kuwa mishale ya huyo Mwenyezi i ndani yangu, Na roho yangu inainywa sumu yake; Vitisho vya Mungu vimejipanga juu yangu. 5 Je! Huyo punda-mwitu hulia akiwa na majani? Au, ng'ombe hulia malishoni? 6 Je! Kitu kisicho na ladha yumkini kulika pasipo chumvi? Au je, uto wa yai una tamu iwayo yote? 7 Roho yangu inakataa hata kuvigusa; Kwangu mimi ni kama chakula kichukizacho. 8 Laiti ningepewa haja yangu, Naye Mungu angenipa neno hilo ninalolitamani sana! 9 Kwamba Mungu angekuwa radhi kuniseta; Kwamba angeulegeza mkono wake na kunikatilia mbali! 10 Hapo ndipo ningefarijika hata sasa; Naam, ningejikuza katika maumivu yasiyoniacha; Kwa kuwa sikuyakana maneno yake Mtakatifu. 11 Nguvu zangu ni zipi, hata ningoje? Na mwisho wangu ni nini, hata nisubiri? 12 Je! Nguvu zangu ni nguvu za mawe? Au mwili wangu, je! Ni shaba? 13 Je! Si kwamba sina msaada ndani yangu. Tena kwamba kufanikiwa kumeondolewa mbali nami? 14 Kwake huyo atakaye kuzima roho inapasa atendewe mema na rafiki; Hata kwake huyo aachaye kumcha Mwenyezi. 15 Ndugu zangu wametenda udanganyifu kama kijito cha maji. Mfano wa fumbi la vijito vipitavyo. 16 Vilivyokuwa vyeusi kwa sababu ya barafu, Ambamo theluji hujificha. 17 Wakati vipatapo moto hutoweka; Kukiwako hari, hukoma mahali pao. 18 Misafara isafiriyo kwa njia yao hugeuka; Hukwea kwenda barani, na kupotea. 19 Misafara ya Tema huvitazama, Majeshi ya Sheba huvingojea. 20 Wametahayari kwa sababu walitumaini; Wakaja huku, nao walifadhaika. 21 Kwani sasa ninyi mmekuwa vivyo; Mwaona jambo la kutisha, mkaogopa. 22 Je! Nilisema, Nipeni? Au, Nitoleeni toleo katika mali yenu? 23 Au, Niokoeni na mkono wa adui? Au, Nikomboeni na mikono ya hao waoneao? 24 Nifunzeni, nami nitanyamaa kimya; Mkanijulishe ni jambo gani nililokosa. 25 Jinsi yafaavyo maneno ya uelekevu! Lakini kuhoji kwenu, je! Kumeonya nini? 26 Je! Mwafikiri kuyakemea maneno? Maana maneno ya huyo aliyekata tamaa ni kama upepo. 27 Naam, mwapenda kuwapigia kura hao mayatima, Na kufanya biashara ya rafiki yenu. 28 Sasa basi iweni radhi kuniangalia; Kwani hakika sitanena uongo usoni penu. 29 Rudini, nawasihi, lisiwe neno la udhalimu; Naam, rudini tena, neno langu ni la haki. 30 Je! Mna udhalimu ulimini mwangu? Je! Makaakaa yangu hayatambui mambo ya madhara?

Ayubu 7

1 Je! Mtu hana wakati wake wa vita juu ya nchi? Na siku zake, je! Si kama siku za mwajiriwa? 2 Kama mtumishi atamaniye sana kile kivuli, Kama mwajiriwa anayetazamia mshahara wake; 3 Ni vivyo nami nimepewa miezi ya ubatili iwe fungu langu, Nami nimeandikiwa masiku yenye kuchokesha. 4 Hapo nilalapo chini, nasema, Nitaondoka lini? Lakini usiku huwa mrefu; Nami nimejawa na kujitupa huku na huku hata kupambazuke. 5 Mwili wangu unavikwa mabuu na madongoa ya udongo; Ngozi yangu hufumba, kisha ikatumbuka tena. 6 Siku zangu hupita upesi kuliko chombo cha kufumia, Nazo zapita pasipokuwa na matumaini. 7 Kumbuka ya kwamba maisha yangu ni upepo; Jicho langu halitaona mema tena. 8 Jicho lake huyo anionaye halitaniangalia tena; Macho yako yatanielekea, lakini sitakuwapo. 9 Kama vile wingu likomavyo na kutoweka, Ni vivyo huyo ashukaye kuzimuni hatazuka tena kabisa. 10 Hatarudi tena nyumbani kwake, Wala mahali pake hapatamjua tena. 11 Kwa hiyo sitakizuia kinywa changu; Nitanena kwa mateso ya roho yangu; Nitalia kwa uchungu wa nafsi yangu. 12 Je! Mimi ni bahari, au je! Ni nyangumi? Hata ukawaweka walinzi juu yangu? 13 Hapo nisemapo, kitanda changu kitanituza moyo, Malazi yangu yatanipunguzia kuugua kwangu; 14 Ndipo unitishapo kwa ndoto, Na kunitia hofu kwa maono; 15 Hata nafsi yangu huchagua kunyongwa, Na kuchagua kifo kuliko maumivu yangu haya. 16 Ninadhoofika; sitaishi sikuzote; Usinisumbue, kwani siku zangu ni uvuvio. 17 Je! Mtu ni kitu gani, hata ukamtukuza, Na kumtia moyoni mwako, 18 Na kumwangalia kila asubuhi, Na kumjaribu kila dakika? 19 Je! Hata lini hukomi kuniangalia; Wala kunisumbua hata nimeze mate? 20 Kwamba nimefanya dhambi, nikufanyieje Ee mlinda wanadamu? Mbona umeniweka niwe shabaha yako, Hata nimekuwa mzigo kwa nafsi yangu? 21 Nawe, je! Mbona hunisamehe makosa yangu, Na kuniondolea maovu yangu? Kwa kuwa sasa nitalala mavumbini; Nawe utanitafuta kwa bidii, lakini sitakuwapo.

Ayubu 8

1 Ndipo Bildadi huyo Mshuhi akajibu, na kusema, 2 Wewe utanena maneno haya hata lini? Maneno ya kinywa chako yatakuwa kama upepo mkuu hata lini? 3 Je! Mungu hupotosha hukumu? Au, huyo Mwenyezi hupotosha yaliyo ya haki? 4 Kwamba watoto wako wamemfanyia dhambi, Naye amewatia mkononi mwa kosa lao; 5 Wewe ukimtafuta Mungu kwa bidii, Na kumsihi huyo Mwenyezi; 6 Ukiwa wewe u safi na mwelekevu; Hakika yeye sasa angeamka kwa ajili yako, Na kuyafanya makazi ya haki yako kufanikiwa. 7 Tena ujapokuwa huo mwanzo wako ulikuwa ni mdogo, Lakini mwisho wako ungeongezeka sana. 8 Basi, uwaulize, tafadhali, vizazi vya zamani, Ujitie kuyaangalia yale baba zao waliyoyatafuta; 9 (Kwani sisi tu wa jana tu, wala hatujui neno, Kwa kuwa siku zetu duniani ni kivuli tu;) 10 Je! Hawatakufunza wao, na kukueleza, Na kutamka maneno yatokayo mioyoni mwao? 11 Je! Hayo mafunjo yamea pasipo matope Na makangaga kumea pasipo maji? 12 Yakiwa yakali mabichi bado, wala hayakukatwa, Hunyauka mbele ya majani mengine. 13 Ndivyo ulivyo mwisho wa hao wamsahauo Mungu; Na matumaini yake huyo mbaya huangamia; 14 Uthabiti wake utavunjika, Na matumaini yake huwa ni nyuzi za buibui. 15 Ataitegemea nyumba yake, isisimame; Atashikamana nayo, isidumu. 16 Yeye huwa mti mbichi mbele ya jua, Nayo machipukizi yake huenea katika bustani yake. 17 Mizizi yake huzonga-zonga chuguu, Huangalia mahali penye mawe. 18 Lakini, aking'olewa mahali pake, Ndipo patamkana, na kusema, Mimi sikukuona. 19 Tazama, furaha ya njia yake ni hii, Na wengine watachipuka kutoka katika nchi. 20 Tazama, Mungu hatamtupa mtu mkamilifu, Wala hatawathibitisha watendao uovu. 21 Bado atakijaza kinywa chako kicheko, Na midomo yako ataijaza shangwe. 22 Hao wakuchukiao watavikwa aibu; Nayo hema yake mwovu haitakuwako tena.

Ayubu 9

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Kweli najua kuwa ndivyo hivyo; Lakini mtu huwaje mwenye haki mbele za Mungu? 3 Kama akipenda kushindana naye, Hawezi kumjibu neno moja katika elfu. 4 Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu; Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa? 5 Aiondoaye milima, nayo haina habari, Akiipindua katika hasira zake. 6 Aitikisaye dunia itoke mahali pake, Na nguzo zake hutetema. 7 Aliamuruye jua, nalo halichomozi; Nazo nyota huzipiga muhuri. 8 Ambaye peke yake ni mwenye kuzitandika mbingu, Na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. 9 Yeye afanyaye hizo nyota za Dubu, na Orioni, na hicho Kilimia, Na makundi ya nyota ya kusini. 10 Atendaye mambo makuu yasiyotafutikana; Naam, mambo ya ajabu yasiyohesabika. 11 Tazama, yuaenenda karibu nami, nisimwone; Tena yuapita kwenda mbele, nisimtambue. 12 Tazama, yuakamata, ni nani awezaye kumzuia? Ni nani awezaye kumwuliza, Wafanya nini? 13 Mungu haondoi hasira zake; Hao wamsaidiao Rahabu huinama chini yake. 14 Je! Mimi nitamjibuje, Na kuyachagua maneno yangu kuhojiana naye? 15 Ambaye, nijapokuwa mimi ni mwenye haki, nisingemjibu; Ningemsihi-sihi mtesi wangu. 16 Kama ningemwita, naye akaniitikia; Hata hivyo singeamini kuwa amesikiza sauti yangu. 17 Yeye anipondaye kwa dhoruba, Na kuziongeza jeraha zangu pasipokuwa na sababu. 18 Haniachi nipate kuvuta pumzi, Lakini hunijaza uchungu. 19 Kama tukitaja nguvu za mashujaa, tazama yupo hapo! Kama tukitaja hukumu, ni nani atakayeniwekea muhula? 20 Ingawa ni mwenye haki, kinywa changu mwenyewe kitanihukumu; Ingawa ni mkamilifu, kitanishuhudia kuwa ni mpotovu. 21 Mimi ni mkamilifu; siangalii nafsi yangu; Naudharau uhai wangu. 22 Hayo yote ni mamoja; kwa hiyo nasema, Yeye huangamiza wakamilifu na waovu pia. 23 Kama hilo pigo likiua ghafula, Atayadhihaki majaribu yake asiye na kosa. 24 Dunia imetiwa mkononi mwa waovu; Yeye hufunika nyuso za waamuzi wake; Kama si yeye, ni nani basi? 25 Basi siku zangu zina mbio kuliko tarishi; Zakimbia, wala hazioni mema. 26 Zimepita kama merikebu ziendazo mbio; Mfano wa tai ayashukiaye mawindo. 27 Nikisema, Mimi nitasahau kuugua kwangu, Nitaacha kununa uso nikachangamke moyo; 28 Mimi huziogopa huzuni zangu zote, Najua kuwa hutanihesabu kuwa sina hatia. 29 Nitahukumiwa kuwa ni mkosa; Ya nini basi nitaabike bure? 30 Ingawaje najiosha kwa maji ya theluji, Na kuitakasa mikono yangu kwa sabuni; 31 Lakini utanitupa shimoni, Nami hata nguo zangu zitanichukia. 32 Kwani yeye si mtu, kama mimi, hata nimjibu, Hata tukaribiane katika hukumu. 33 Hapana mwenye kuamua katikati yetu, Awezaye kutuwekea mkono sote wawili. 34 Na aniondolee fimbo yake, Na utisho wake usinitie hofu; 35 Ndipo hapo ningesema, nisimwogope; Kwani sivyo nilivyo nafsini mwangu.

Ayubu 10

1 Nafsi yangu inachoka na maisha yangu; Sitajizuia na kuugua kwangu; Nitanena kwa uchungu wa roho yangu. 2 Nitamwambia Mungu, Usinihukumie makosa; Nionyeshe sababu ya wewe kushindana nami. 3 Je! Ni vema kwako wewe kuonea, Na kuidharau kazi ya mikono yako, Na kuyaangazia mashauri ya waovu? 4 Je! Wewe una macho ya kimwili, Au je! Waona kama aonavyo binadamu? 5 Je! Siku zako ni kama siku za mtu, Au je! Miaka yako ni kama siku za mtu, 6 Hata ukauliza-uliza habari za uovu wangu, Na kuitafuta dhambi yangu, 7 Ujapojua ya kuwa mimi si mwovu; Wala hapana awezaye kuokoa na mkono wako? 8 Mikono yako imeniumba na kunifinyanga; Nawe utageuka na kuniangamiza? 9 Kumbuka, nakusihi ulivyonifinyanga kama vile udongo; Nawe, je! Utanirudisha uvumbini tena? 10 Je! Wewe hukunimimina kama maziwa, Na kunigandisha mfano wa jibini? 11 Umenivika ngozi na nyama, Na kuniunga pamoja kwa mifupa na mishipa. 12 Umenijazi uhai na upendeleo, Na maangalizi yako yameilinda roho yangu. 13 Lakini mambo haya uliyaficha moyoni mwako; Najua kuwa haya yamo nafsini mwako; 14 Nikifanya dhambi, ndipo waniangalia, Wala hutaniachilia na uovu wangu. 15 Mimi nikiwa mbaya, ole wangu! Nami nikiwa mwenye haki, walakini sitainua kichwa changu; Mimi nimejaa aibu Na kuyaangalia mateso yangu. 16 Kichwa changu kikijiinua, waniwinda kama simba; Tena wajionyesha kwangu kuwa wa ajabu. 17 Wewe warejeza upya hao mashahidi yako juu yangu, Na kasirani yako waiongeza juu yangu; Jeshi kwa jeshi juu yangu. 18 Kwa nini basi kunitoa tumboni? Ningekata roho, lisinione jicho lo lote. 19 Ningalikuwa kama mtu asiyekuwapo; Ningalichukuliwa kaburini kutoka tumboni. 20 Je! Siku zangu si chache? Acha basi, Usinisumbue, nipate ngaa kutuzwa moyo kidogo. 21 Kabla sijaenda huko ambako sitarudi kutoka huko tena, Ni hiyo nchi ya giza, giza tupu; 22 Ni nchi ya giza kuu, kama giza lenyewe lilivyo; Ni nchi ya giza tupu, isiyo na matengezo ya mambo yo yote, Nchi ambayo nuru yake ni kama giza.

Ayubu 11

1 Ndipo Sofari Mnaamathi akajibu, na kusema, 2 Je! Huu wingi wa maneno usijibiwe? Na mtu aliyejaa maneno, je! Ahesabiwe kuwa na haki? 3 Je! Majivuno yako yawanyamazishe watu wawe kimya? Nawe hapo ufanyapo dhihaka, je! Hapana mtu atakayekutahayarisha? 4 Kwa kuwa wewe wasema, Mafunzo yangu ni safi, Nami ni safi machoni pako. 5 Lakini, laiti Mungu angenena, Na kuifunua midomo yake juu yako; 6 Tena akuonyeshe hizo siri za hekima, Ya kuwa hufanikiwa katika kuyatimiza makusudi yake! Ujue basi ya kuwa Mungu akuachilia katika uovu wako. 7 Je! Wewe waweza kuuvumbua ukuu wa Mungu? Waweza kuufikilia upeo wa huyo Mwenyezi? 8 Ni juu mno kama mbingu; waweza kufanya nini wewe? Ni wenye kina kuliko kuzimuni; waweza kujua nini wewe? 9 Cheo chake ni kirefu kuliko dunia, Ni kipana zaidi ya bahari. 10 Yeye akipita, na kufunga watu, Na kuwaita hukumuni, ni nani basi awezaye kumzuia? 11 Kwani yeye awajua watu baradhuli; Huona na uovu pia, hata asipoufikiri. 12 Lakini mpumbavu aweza kupata ufahamu, Ingawa mwanadamu huzaliwa kama mtoto wa punda-mwitu. 13 Wewe ukiuweka moyo wako kwa uelekevu, Na kumnyoshea mikono yako; 14 Ikiwa una uovu mkononi mwako, uweke mbali nawe, Wala usikubali upuzi kukaa hemani mwako; 15 Hakika ndipo utakapopata kuinua uso pasipo ila; Naam, utathibitika, wala hutakuwa na hofu; 16 Kwa kuwa utasahau mashaka yako; Utayakumbuka kama maji yaliyokwisha pita; 17 Na maisha yako yatakuwa meupe kuliko adhuhuri; Lijapokuwa ni giza, litakuwa kama alfajiri. 18 Nawe utakuwa salama, kwa sababu kuna matumaini; Naam, utatafuta-tafuta kando yako, na kupumzika katika salama. 19 Tena utalala, wala hapana atakayekutia hofu; Naam, wengi watakutafuta uso wako. 20 Lakini macho ya waovu yataingia kiwi, Nao hawatakuwa na njia ya kukimbilia, Na matumaini yao yatakuwa ni kutoa roho.

Ayubu 12

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Hapana shaka ninyi ndinyi watu halisi, Nanyi mtakapokufa, ndipo na hekima itakoma. 3 Lakini mimi pia, nina fahamu kama ninyi; Mimi si duni yenu ninyi; Naam, ni nani asiyejua mambo kama hayo? 4 Mimi ni mtu wa kuchekwa na jirani yake, Ni mtu niliyemwita Mungu, naye akanijibu; Huyo mwenye haki, aliye mtimilifu, amekuwa ni kicheko. 5 Katika mawazo yake huyo aliye na raha mna kudharau mashaka; Tayari kwa ajili ya wenye kuteleza miguu. 6 Hema za wapokonyi hufanikiwa, Na hao wamkasirishao Mungu hukaa salama; Mikononi mwao Mungu huleta vitu vingi. 7 Lakini sasa waulize hao wanyama, nao watakufundisha; Na nyuni wa angani, nao watakuambia; 8 Au nena na nchi, nayo itakufundisha; Nao samaki wa baharini watakutangazia. 9 Katika hawa wote ni yupi asiyejua, Kwamba ni mkono wa Bwana uliofanya haya? 10 Ambaye nafsi ya kila kilicho hai i mkononi mwake, Na pumzi zao wanadamu wote. 11 Je! Sikio silo lijaribulo maneno, Kama vile kaakaa lionjavyo chakula? 12 Wazee ndio walio na hekima, Na katika kuishi siku nyingi iko fahamu. 13 Hekima na amri zina yeye [Mungu]; Yeye anayo mashauri na fahamu. 14 Tazama, yuavunja, wala haiwezekani kujenga tena; Humfunga mtu, wala haiwezekani kumfungua. 15 Tazama, yuayazuia maji, nayo yakatika; Tena, huyapeleka, nayo yaipindua dunia. 16 Kwake yeye ziko nguvu, na makusudi kufanikiwa; Huyo adanganywaye, na mdanganyi pia ni wake. 17 Yeye huwaondoa washauri hali wametekwa nyara, Naye huwafanya waamuzi kuwa ni wapumbavu. 18 Yeye hulegeza kifungo cha wafalme, Na kuwafunga viuno vyao kwa mshipi. 19 Yeye huwaondoa makuhani hali wametekwa nyara. Na kuwapindua mashujaa. 20 Huondoa matamko ya hao walioaminiwa, Na kuondoa fahamu za wazee. 21 Humwaga aibu juu ya hao wakuu, Na kulegeza mshipi wa wenye nguvu. 22 Huvumbua mambo ya siri tokea gizani, Na hicho kilicho giza tupu huleta mwangani. 23 Huyaongeza mataifa, na kuyaangamiza; Huyaeneza mataifa mbali, na kuyaacha. 24 Huwaondolea moyo wakuu wa watu wa nchi, Na kuwapoteza nyikani pasipokuwa na njia. 25 Wao hupapasa gizani pasipokuwa na mwanga, Naye huwafanya kupepesuka kama vile mlevi.

Ayubu 13

1 Tazama, jicho langu limeyaona hayo yote, Sikio langu limeyasikia na kuelewa nayo. 2 Hayo myajuayo ninyi, na mimi pia nayajua; Mimi si duni kuliko ninyi. 3 Hakika ningenena naye huyo Mwenyezi, Nami nataka kuhojiana na Mungu. 4 Lakini ninyi hubuni maneno ya uongo, Ninyi nyote ni matabibu wasiofaa. 5 Laiti mngenyamaza kabisa! Hilo lingekuwa hekima kwenu. 6 Sikieni sasa basi hoja zangu, Mkayasikie mashindano ya midomo yangu. 7 Je! Mtanena yasiyo ya haki kwa ajili ya Mungu, Na kusema kwa udanganyifu kwa ajili yake? 8 Je! Mtamwonyesha yeye upendeleo? Mtamtetea Mungu? 9 Je! Itafaa yeye kuwatafuta ninyi? Au, kama kumdanganya mtu, je! Mtamdanganya yeye? 10 Hakika atawakemea ninyi, Mkiwapendelea watu kwa siri. 11 Je! Huo ukuu wake hautawatia hofu, Na utisho wake hautawaangukia? 12 Matamko yenu ya hekima ni mithali ya majivu, Ngome zenu ni ngome za udongo. 13 Nyamazeni, niacheni, ili nipate kunena, Na hayo yatakayonijilia na yaje. 14 Nitaitwaa nyama ya mwili wangu katika meno yangu, Na kuutwaa uhai wangu mkononi mwangu! 15 Tazama, ataniua; sina tumaini; ila hata hivyonitaithibitisha njia yangu mbele yake. 16 Hili nalo litakuwa ni wokovu wangu; Kwani asiyemcha Mungu hatakaribia mbele yake. 17 Sikieni sana maneno yangu, Maelezo yangu na yaingie masikioni mwenu. 18 Angalieni sasa, nimekwisha kulitengeneza neno langu, Najua ya kuwa ni mwenye haki mimi. 19 Yuko nani atakayeshindana nami? Maana sasa nitanyamaa kimya na kutoa roho. 20 Lakini msinifanyie mambo mawili, hayo tu, Ndipo nami sitajificha usoni pako; 21 Uondoe mkono wako usinilemee; Na utisho wako usinitie hofu. 22 Basi uite wakati huo, nami nitaitika; Au, niache ninene mimi, nawe unijibu. 23 Maovu yangu na dhambi zangu ni ngapi? Nijulishe kosa langu na dhambi yangu. 24 Mbona umeuficha uso wako, Na kunihesabu kuwa ni adui yako? 25 Je! Utalitaabisha jani lipeperushwalo? Au, je! Utayafuatia hayo mabua makavu? 26 Kwani umeandika maneno ya uchungu juu yangu, Na kunirithisha maovu ya ujana wangu; 27 Waitia miguu yangu katika mkatale, na kuyaaua mapito yangu yote; Wajiandikia alama kuzizunguka nyayo za miguu yangu; 28 Nijapokuwa ni kama kitu kilichooza, kinachosinyaa, Mfano wa nguo iliyoliwa na nondo.

Ayubu 14

1 Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. 2 Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; Hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe. 3 Nawe, je! Wafumbua macho yako kumwangalia mtu kama yeye, Na kunitia katika hukumu pamoja nawe? 4 Ni nani awezaye kutoa kitu kilicho safi kitoke katika kitu kichafu? Hapana awezaye. 5 Kwa kuwa siku zake zimeamriwa, hesabu ya miezi yake unayo wewe, Nawe umemwekea mipaka yake asiyoweza kuipita; 6 Acha kumwangalia yeye, apate kupumzika, Hata atakapoitimiza siku yake, kama aliyeajiriwa. 7 Kwani yako matumaini ya mti, ya kuwa ukikatwa utachipuka tena, Wala machipukizi yake hayatakoma. 8 Ijapokuwa mizizi yake huchakaa mchangani, Na shina lake kufa katika udongo; 9 Lakini kwa harufu ya maji utachipuka, Na kutoa matawi kama mche. 10 Lakini mwanadamu hufa, huifariki dunia; Naam, mwanadamu hutoa roho, naye yupo wapi? 11 Kama vile maji kupwa katika bahari, Na mto kupunguka na kukatika; 12 Ni vivyo mwanadamu hulala chini, asiinuke; Hata wakati wa mbingu kutokuwako tena, hawataamka, Wala kuamshwa usingizini. 13 Laiti ungenificha kuzimuni, Ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita, Na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka! 14 Mtu akifa, je! Atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, Hata kufunguliwa kwangu kunifikilie. 15 Wewe ungeita, nami ningekujibu; Ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako. 16 Lakini sasa wazihesabu hatua zangu; Je! Huchungulii dhambi yangu? 17 Kosa langu limetiwa muhuri mfukoni, Nawe waufunga uovu wangu. 18 Lakini, tazama, mlima ukianguka hutoweka, Nalo jabali huondolewa mahali pake; 19 Maji mengi huyapunguza mawe; Mafuriko yake huuchukua mchanga wa nchi; Nawe matumaini ya wanadamu wayaangamiza. 20 Wewe wamshinda nguvu sikuzote, naye hupita aende zake Wabadili sura zake, na kumpeleka aondoke. 21 Wanawe hufikilia heshima, wala yeye hajui; Kisha wao huaibishwa, lakini yeye hana habari zao. 22 Lakini mwili ulio juu yake una maumivu, Na nafsi yake ndani huomboleza.

Ayubu 15

1 Ndipo Elifazi, Mtemani, akajibu, na kusema, 2 Je! Yapasa mtu mwenye hekima kujibu kwa ujuzi wa uvuvio, Na kujaza tumbo lake na upepo wa mashariki? 3 Je! Ahoji na mazungumzo yasiyo faida, Au kwa maneno ambayo hawezi kufanya mema kwayo? 4 Naam, wewe waondoa kicho, Nawe wazuia ibada mbele za Mungu. 5 Kwani uovu wako unakufundisha kinywa chako, Nawe wachagua ulimi wake mwenye hila. 6 Kinywa chako mwenyewe chakuhukumia makosa, wala si mimi; Naam, midomo yako mwenyewe hushuhudia juu yako. 7 Je! Wewe u mtu wa kwanza aliyezaliwa? Au, ulizawa wewe kabla ya milima? 8 Je! Umesikia mashauri ya siri ya Mungu? Nawe je! Wazuia hekima iwe yako tu? 9 Je! Wewe wajua neno lipi, ambalo sisi hatulijui? Nawe wafahamu nini, ambalo halimo ndani yetu? 10 Wenye mvi, na walio wazee sana, wote wapo pamoja nasi, Ambao ni wazee kuliko baba yako. 11 Je! Utulizi wa Mungu ni mdogo sana kwako, Na hilo neno la upole si kitu kwako? 12 Mbona moyo wako unakutaharakisha! Na macho yako, je! Kwani kung'ariza? 13 Hata ukageuza roho yako iwe kinyume cha Mungu, Na kuyatoa maneno kama hayo kinywani mwako. 14 Je! Mwanadamu ni kitu gani, hata akawa safi? Huyo aliyezaliwa na mwanamke, hata awe na haki? 15 Yeye hawategemei watakatifu wake; Naam, mbingu nazo si safi machoni pake. 16 Sembuse mtu ambaye ni mwenye kuchukiza na uchafu, Mwanadamu anywaye uovu kama anywavyo maji! 17 Mimi nitakuonyesha, unisikilize; Na hayo yote niliyoyaona nitayanena; 18 (Ambayo watu wenye hekima wameyatangaza Tokea baba zao, wala hawakuyaficha; 19 Waliopewa hiyo nchi peke yao, Wala mgeni hakupita kati yao); 20 Mtu mwovu huwa na uchungu siku zake zote, Hata hesabu ya miaka aliyowekewa mwenye kuonea. 21 Sauti za utisho zi masikioni mwake; Katika kufanikiwa kwake mtekaji nyara atamjia juu yake; 22 Yeye hasadiki kwamba atarudi kutoka gizani, Naye hungojewa na upanga; 23 Hutanga-tanga ili apate chakula, akisema, Ki wapi? Ajua kwamba siku ya giza i tayari karibu yake; 24 Mateso na dhiki humtia hofu; Humshinda kama vile mfalme aliye tayari kwa vita; 25 Kwa kuwa amenyosha mkono wake juu ya Mungu, Na kuendelea kwa kiburi kinyume cha Mwenyezi; 26 Humshambulia na shingo ngumu, Kwa mafundo makubwa ya ngao zake; 27 Kwa kuwa amefunika uso wake na kunona kwake, Na kuwandisha mafuta kiunoni mwake; Naye amekaa katika miji iliyo ukiwa, 28 Katika nyumba ambazo hapana mtu azikaaye, Zilizokuwa tayari kuwa magofu. 29 Hatakuwa tajiri, wala mali zake hazitadumu, Wala maongeo yao hayatainama nchi. 30 Hataondoka gizani; Ndimi za moto zitayakausha matawi yake, Naye ataondoka kwa pumzi za kinywa chake. 31 Asiutumainie ubatili, na kujidanganya; Kwa kuwa huo ubatili ndio utakaokuwa ujira wake. 32 Jambo hili litatendeka kabla ya wakati wake, Na tawi lake halitasitawi. 33 Atayapukutisha mapooza yake kama mzabibu, Na kuyatupa maua yake kama mzeituni. 34 Kwa kuwa jamii ya hao wasiomcha Mungu watakuwa tasa, Na moto utateketeza mahema yenye rushwa. 35 Wao hutunga mimba ya madhara, na kuzaa uovu, Nalo tumbo lao hutengeza udanganyifu.

Ayubu 16

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Nimesikia maneno mengi mfano wa hayo; Ninyi nyote ni wafariji wenye kutaabisha. 3 Je! Maneno yasiyo faida yatakuwa na mwisho? Au, kuna nini kinachokukasirisha, hata ukajibu? 4 Mimi nami ningeweza kunena kama ninyi; Kama roho zenu zingekuwa mahali pa roho yangu, Ningeweza kutunga maneno juu yenu, Na kuwatikisia ninyi kichwa changu. 5 Lakini ningewatia nguvu kwa kinywa changu, Na utuzo wa midomo yangu ungetuliza. 6 Nijapokuwa nanena, huzuni yangu haitulizwi; Nijapokuwa najizuia, nimepunguziwa kitu gani? 7 Lakini sasa amenichokesha; Jamii yangu yote umeifanya ukiwa. 8 Umenishika sana, ni ushahidi juu yangu; Na kukonda kwangu kwaniinukia, kwanishuhudia usoni pangu. 9 Amenirarua katika ghadhabu zake, na kunionea; Amesaga-saga meno juu yangu; Mtesi wangu hunikazia macho makali. 10 Wamenifumbulia vinywa vyao; Wamenipiga shavuni kwa kunitukana; Hujikutanisha pamoja juu yangu. 11 Mungu amenitia kwa hao wapotovu, Na kunitupa mikononi mwao waovu. 12 Nilikuwa katika raha, naye akanivunja-vunja; Naam, amenishika shingo, na kuniponda; Tena amenisimamisha niwe shabaha yake. 13 Wapigaji wake wa mishale hunizingira kotekote, Hunipasua viuno vyangu, asinihurumie; Nyonga zangu amezimwaga juu ya nchi. 14 Hunivunja kwa uvunjifu juu ya uvunjifu; Hunishambulia mfano wa jitu shujaa. 15 Nimeshona nguo ya magunia juu ya mwili wangu, Na pembe yangu nimeidhili uvumbini. 16 Uso wangu umeharibika kwa kutoa machozi, Na giza tupu li katika kope zangu; 17 Ijapokuwa hapana jeuri mikononi mwangu, Na kuomba kwangu ni safi. 18 Ee nchi, usiifunike damu yangu, Na kilio changu kisipate mahali pa kupumzika. 19 Hata sasa, tazama, shahidi wangu yuko mbinguni. Na huyo atakayenidhamini yuko juu. 20 Rafiki zangu hunidharau; Lakini jicho langu humwagia Mungu machozi; 21 Laiti angemtolea mtu hoja mbele ya Mungu, Amtetee na mwanadamu mbele ya jirani yake. 22 Kwani ikiisha pita miaka michache, Nitakwenda njia hiyo ambayo sitarudi tena.

Ayubu 17

1 Roho yangu imezimika, siku zangu zimekoma, Kaburi i tayari kunipokea. 2 Ni kweli wako kwangu wenye kufanya dhihaka, Jicho langu hukaa katika kunifanyia uchungu kwao. 3 Nipe rehani basi, uwe dhamana kwa ajili yangu kwako wewe mwenyewe; Kuna nani atakayeniwekea dhamana? 4 Kwani mioyo yao imeificha ufahamu; Kwa hiyo hutawakuza. 5 Awafitiniye rafiki zake wawe mawindo, Hata macho ya watoto wake yataingia kiwi. 6 Amenifanya niwe simo kwa watu; Nimekuwa mwenye kuchukiwa kwa wazi. 7 Jicho langu nalo limekuwa giza kwa sababu ya majonzi, Na via vyangu vyote vimekuwa kama kivuli. 8 Walekevu watayastaajabia hayo, Na asiye na hatia atajiamsha juu ya mpotovu. 9 Lakini mwenye haki ataishika njia yake, Naye mwenye mikono safi atazidi kupata nguvu. 10 Lakini rudini; ninyi nyote, njoni sasa; Wala sitampata mtu mwenye hekima kati yenu. 11 Siku zangu zimepita, makusudi yangu yamevunjika, Hata hayo niliyo nayo moyoni mwangu. 12 Wabadili usiku kuwa mchana; Wasema, Mwanga u karibu kwa sababu ya giza. 13 Nikitazamia kuzimu kuwa nyumba yangu; Nikitandika malazi yangu gizani; 14 Ikiwa nimeuita uharibifu, Wewe u baba yangu; Na kuliambia buu, Wewe u mama yangu, na umbu langu; 15 Basi, tumaini langu li wapi? Na tumaini langu, ni nani atakayeliona? 16 Litashuka kwenye makomeo ya kuzimu, Itakapokuwapo raha mavumbini.

Ayubu 18

1 Ndipo Bildadi, Mshuhi, akajibu, na kusema, 2 Je! Hata lini utayategea maneno mitambo? Fikiri, kisha baadaye tutanena. 3 Twahesabiwa kuwa wanyama kwa sababu gani, Tena kuwa wanajisi machoni pako? 4 Wewe ujiraruaye mwenyewe katika hasira yako, Je! Dunia itaachwa kwa ajili yako wewe? Au jabali litaondolewa mahali pake? 5 Naam, mwanga wa waovu utazimika, Wala mwali wa moto wake hautang'aa. 6 Mwanga hemani mwake utakuwa giza, Nayo taa iliyo juu yake itazimishwa. 7 Hatua zake za nguvu zitasongwa, Na shauri lake mwenyewe litamwangusha chini. 8 Kwani ametupwa katika wavu na miguu yake mwenyewe, Naye huenda juu ya matanzi. 9 Tanzi litamshika kisigino chake, Na mtambo utamgwia. 10 Amefichiwa tanzi chini, Na mtego amewekewa njiani. 11 Matisho yatamtia hofu pande zote, Na kumfukuza karibu na visigino vyake. 12 Nguvu zake zitaliwa na njaa, Na msiba utakuwa tayari kwa kusita kwake. 13 Utakula via vya mwili wake, Naam, mzaliwa wa kwanza wa mauti atavila via vyake. 14 Atang'olewa katika hema yake aliyokuwa akiitumaini; Naye atapelekwa kwake mfalme wa utisho. 15 Ambacho si chake kitakaa katika hema yake; Kiberiti kitamwagwa juu ya makazi yake. 16 Chini, mizizi yake itakaushwa; Na juu, tawi lake litasinyaa. 17 Kumbukumbu lake litakoma katika nchi, Wala hatakuwa na jina mashambani. 18 Atakimbizwa kutoka mwangani hata gizani, Na kufukuzwa atoke duniani. 19 Hatakuwa na mwana wala mjukuu kati ya watu wake, Wala hatasalia mtu hapo alipokaa. 20 Hao wanaokaa magharibi watastaajabia siku yake, Kama vile wanaokaa mashariki walivyotiwa hofu. 21 Hakika ndivyo yalivyo makazi ya wapotovu, Na hapa ni mahali pake asiyemjua Mungu.

Ayubu 19

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Je! Mtanichukiza nafsi yangu hata lini, Na kunivunja-vunja kwa maneno? 3 Mara kumi hizi mmenishutumu; Hamwoni haya kunifanyia mambo magumu. 4 Ingawaje nimekosa, Kosa langu hukaa kwangu mwenyewe. 5 Kwamba mtajitukuza juu yangu, Na kunena juu yangu shutumu langu; 6 Jueni basi kuwa Mungu amenipotosha, Na kunizingira kwa wavu wake. 7 Tazama, nalia, Udhalimu, lakini sisikiwi; Naulilia msaada, wala hapana hukumu. 8 Yeye ameiziba njia yangu nisipate kupita, Na kutia giza katika mapito yangu. 9 Amenivua utukufu wangu, Na kuiondoa taji kichwani mwangu. 10 Amenibomoa pande zote, nami nimetoweka; Na tumaini langu ameling'oa kama mti. 11 Tena ameziwasha ghadhabu zake juu yangu, Akanihesabia kuwa mmoja katika watesi wake. 12 Majeshi yake husongea pamoja, na kunipandishia njia yao, Na kupiga marago kuizunguka hema yangu. 13 Amewaweka ndugu zangu mbali nami, Na wanijuao wametengwa nami kabisa. 14 Watu wa mbari yangu wamekoma, Na rafiki zangu niwapendao wamenisahau. 15 Wakaao nyumbani mwangu, na vijakazi vyangu, wanihesabu kuwa mgeni; Mimi ni mgeni machoni pao. 16 Namwita mtumishi wangu, wala haniitikii, Ingawa namsihi kwa kinywa changu. 17 Pumzi zangu ni kama za mgeni kwa mke wangu, Nami ni machukizo kwa ndugu zangu. 18 Hata watoto wadogo hunidharau; Nikiondoka, huninena. 19 Wasiri wangu wote wanichukia; Na hao niliowapenda wamenigeukia. 20 Mfupa wangu unagandamana na ngozi yangu na nyama yangu, Nami nimeokoka na ngozi ya meno yangu tu. 21 Nihurumieni, nihurumieni, enyi rafiki zangu, Kwa maana mkono wa Mungu umenigusa. 22 Mbona ninyi mnaniudhi kama Mungu, Wala hamkutosheka na nyama yangu? 23 Laiti maneno yangu yangeandikwa sasa! Laiti yangeandikwa kitabuni! 24 Yakachorwa katika mwamba milele, Kwa kalamu ya chuma na risasi. 25 Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. 26 Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu; 27 Nami nitamwona mimi nafsi yangu, Na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine. Mtima wangu unazimia ndani yangu. 28 Kama mkisema, Jinsi tutakavyomwudhi! Kwa kuwa shina la jambo hili limeonekana kwake; 29 Uogopeni upanga; Kwa maana adhabu za upanga zina ghadhabu, Mpate kujua ya kwamba hukumu iko.

Ayubu 20

1 Ndipo Sofari, Mnaamathi, akajibu, na kusema, 2 Kwa hiyo mawazo yangu hunipa jawabu, Kwa ajili ya haraka niliyo nayo ndani yangu. 3 Nimesikia maonyo yanayonitahayarisha, Nayo roho ya ufahamu wangu hunijibu. 4 Je! Hujui neno hili tangu zamani za kale, Tangu wanadamu kuwekwa juu ya nchi, 5 Ya kuwa shangwe ya waovu ni kwa muda kidogo, Na furaha ya wapotovu ni ya dakika moja tu? 6 Ujapopanda ukuu wake mpaka mbinguni, Na kichwa chake kufikilia mawinguni; 7 Hata hivyo ataangamia milele kama mavi yake mwenyewe; Hao waliomwona watasema, Yuko wapi? 8 Ataruka mfano wa ndoto, asionekane; Naam, atafukuzwa kama maono ya usiku, 9 Jicho lililomwona halitamwona tena; Wala mahali pake hapatamtazama tena. 10 Watoto wake watataka fadhili kwa maskini, Na mikono yake itarudisha mali yake. 11 Mifupa yake imejaa ujana wake, Lakini utalala nchi naye mavumbini. 12 Ingawa uovu una tamu kinywani mwake, Ingawa auficha chini ya ulimi wake; 13 Ingawa auhurumia, asikubali kuuacha uende zake. Lakini akaushika vivyo kinywani mwake; 14 Hata hivyo chakula chake matumboni mwake kinabadilika, Kimekuwa ni nyongo za majoka ndani yake. 15 Amemeza mali, naye atayatapika tena; Mungu atayatoa tumboni mwake. 16 Ataamwa sumu ya majoka; Na ulimi wa fira utamwua. 17 Hataiangalia hiyo mito ya maji, Vile vijito vilivyojaa asali na siagi. 18 Aliyoyataabikia kazi atayarudisha, asiyameze; Kwa mali aliyoyapata, hatafurahi. 19 Kwa maana amewaonea na kuwaacha maskini; Amenyang'anya nyumba kwa jeuri, wala hataijenga. 20 Kwa sababu hakujua utulivu ndani yake, Hataponya cho chote katika hicho alichokifurahia. 21 Hakikusalia kitu asichokula; Kwa hiyo kufanikiwa kwake hakutadumu. 22 Katika kujaa kwa wingi wake atakuwa katika dhiki; Mkono wa kila anayesumbuliwa utamjia. 23 Hapo atakapo kulijaza tumbo lake, Mungu atamtupia ukali wa ghadhabu zake, Na kuunyesha juu yake akiwa anakula. 24 Ataikimbia silaha ya chuma, Na uta wa shaba utamchoma kwa pili. 25 Yeye autoa, nao watoka mwilini mwake; Naam, ncha ing'aayo yatoka katika nyongo yake; Vitisho viko juu yake. 26 Giza lote linawekwa kwa ajili ya hazina zake; Moto ambao haukuvuviwa na mtu utamla; Utayateketeza yaliyosalia hemani mwake. 27 Mbingu zitafunua wazi uovu wake, Nayo nchi itainuka kinyume chake. 28 Maongeo ya nyumba yake yataondoka, Yatamwagika mbali katika siku ya ghadhabu zake. 29 Hii ndiyo sehemu ya mtu mwovu itokayo kwa Mungu, Na urithi aliowekewa na Mungu.

Ayubu 21

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Yasikizeni sana maneno yangu; Jambo hili na liwe faraja yenu. 3 Niacheni, nami pia nitanena; Tena nikiisha nena, zidini kudhihaki. 4 Mimi, je! Mashitaka yangu yamhusu mwanadamu? Nami kwa nini nisikose kusubiri? 5 Niangalieni, mkastaajabu, Mkaweke mkono kinywani. 6 Hata nikumbukapo nahuzunika, Na utisho wanishika mwilini mwangu. 7 Mbona waovu wanaishi, Na kuwa wazee, naam, na kuongezeka kuwa na nguvu? 8 Kizazi chao kinathibitika nao machoni pao, Na wazao wao mbele ya macho yao. 9 Nyumba zao zi salama pasina hofu, Wala fimbo ya Mungu haiwapigi. 10 Fahali wao huvyaza wala hapungukiwi na nguvu; Ng'ombe wao mke huzaa, asiharibu mimba. 11 Huwatoa kama kundi watoto wao. Na watoto wao hucheza. 12 Huimba kwa matari na kwa kinubi, Na kuifurahia sauti ya filimbi. 13 Siku zao hutumia katika kufanikiwa, Kisha hushuka kuzimuni ghafula. 14 Walakini walimwambia Mungu. Tuondokee; Kwani hatutaki kuzijua njia zako. 15 Huyo Mwenyezi ni nani, hata tumtumikie? Nasi tutafaidiwa nini tukimwomba? 16 Tazama, kufanikiwa kwao hakumo mkononi mwao; Mashauri ya waovu na yawe mbali nami. 17 Je! Ni mara ngapi taa yao waovu huzimishwa? Na msiba wao kuwajilia? Na Mungu kuwagawanyia uchungu kwa hasira yake? 18 Ili wawe kama mabua makavu mbele ya upepo, Kama makapi yaliyochukuliwa na dhoruba? 19 Mwasema, Mungu huwawekea watoto wa mtu huo uovu wake. Na amlipe mwenyewe, ili apate kuujua. 20 Macho yake mwenyewe na yaone uharibifu wake, Akanywe ghadhabu zake Mwenyezi. 21 Kwani ana furaha gani katika mbari yake baada yake, Hesabu ya miezi yake itakapokwisha katwa katikati? 22 Je! Mtu awaye yote atamfundisha Mungu maarifa? Naye ndiye awahukumuye walioko juu. 23 Mmoja hufa katika nguvu zake kamili, Mwenye kukaa salama na kustarehe; 24 Vyombo vyake vimejaa maziwa, Na mafuta ya mifupani mwake ni laini. 25 Mwingine hufa katika uchungu wa roho, Asionje mema kamwe. 26 Wao hulala mavumbini sawasawa, Mabuu huwafunika. 27 Tazama, nayajua mawazo yenu, Na mashauri mnayoazimia kwa uovu juu yangu. 28 Kwa kuwa mwasema, Nyumba ya huyo mkuu i wapi? Na hema waliyoikaa hao waovu i wapi? 29 Je! Hamkuwauliza wapitao njiani? Na maonyo yao hamyajui? 30 Kwamba mwovu huachiliwa katika siku ya msiba? Na kuongozwa nje katika siku ya ghadhabu? 31 Ni nani atakayetangaza njia yake usoni pake? Tena ni nani atakayemlipa kwa hayo aliyofanya? 32 Pamoja na hayo atachukuliwa kaburini, Nao watalinda zamu juu ya ziara lake. 33 Udongo wa bondeni utakuwa tamu kwake, Na watu wote watafuata nyuma yake, Kama vile walivyomtangulia watu wasiohesabika. 34 Basi imekuwaje ninyi kunituza moyo bure, Kwa kuwa katika jawabu zenu unasalia uongo tu.

Ayubu 22

1 Ndipo huyo Elifazi Mtemani akajibu, na kusema, 2 Je! Yumkini mtu awaye yote kumfaa Mungu? Hakika yeye aliye na hekima hujifaa mwenyewe. 3 Je! Mwenyezi hupata furaha katika wewe kuwa mwenye haki? Au je, ni faida kwake, kwamba wafanya njia zako kuwa timilifu? 4 Je! Ni kwa wewe kumcha yeye anakukemea? Na kuingia hukumuni nawe? 5 Je! Uovu wako si mkuu? Wala maovu yako hayana mwisho. 6 Kwa kuwa umetwaa dhamana kwa nduguyo bure, Na kuwavua nguo zao walio uchi. 7 Hukumpa maji ya kunywa huyo aliyechoka, Nawe umemnyima chakula huyo mwenye njaa. 8 Lakini huyo shujaa, nchi ilikuwa yake; Na huyo mwenye kusifiwa, yeye aliikaa. 9 Umewafukuza wanawake wajane hali ya utupu, Na mikono ya mayatima imevunjwa. 10 Kwa hiyo umezungukwa na mitego, Na hofu ya ghafula yakutaabisha, 11 Au je! Huoni giza, Na maji mengi yanayokufunika? 12 Je! Mungu hayuko mbinguni juu? Tena tazama umbali wa nyota, jinsi zilivyo juu! 13 Nawe wasema, Mungu anajua nini? Je! Aweza kuamua kati ya giza kuu? 14 Mawingu mazito ni kifuniko chake, hata asione; Naye yuatembea juu ya kuba ya mbingu. 15 Je! Utaiandama njia ya zamani Waliyoikanyaga watu waovu? 16 Ambao walinyakuliwa kabla ya wakati wao, Msingi wao ulimwagika kama kijito cha maji; 17 Waliomwambia Mungu, Tuondokee; Tena, Huyo Mwenyezi aweza kutufanyia nini? 18 Naye ndiye aliyezijaza nyumba zao vitu vyema; Lakini mashauri ya waovu na yawe mbali nami. 19 Wenye haki huyaona hayo wakafurahi; Nao wasio na hatia huwacheka; 20 Wasema, Hakika hao waliotuinukia wamekatiliwa mbali, Na mabaki yao moto umeyateketeza. 21 Mjue sana Mungu, ili uwe na amani; Ndivyo mema yatakavyokujia. 22 Uyapokee, tafadhali, mafunzo yatokayo kinywani mwake, Na maneno yake yaweke moyoni mwako. 23 Ukimrudia Mwenyezi, utajengwa; Ukiuondoa udhalimu mbali na hema yako. 24 Nawe hazina zako ziweke mchangani, Na dhahabu ya Ofiri iweke kati ya mawe ya vijito; 25 Naye Mwenyezi atakuwa hazina yako, Atakuwa ni fedha ya thamani kwako. 26 Kwani ndipo utakapojifurahisha katika Mwenyezi, Na kuinua uso wako kumwelekea Mungu. 27 Utamwomba yeye naye atakusikia; Nawe utazitimiliza nadhiri zako. 28 Nawe utakusudia neno, nalo litathibitika kwako; Na mwanga utaziangazia njia zako. 29 Hapo watakapokuangusha, utasema, Kuna kuinuka tena; Naye mnyenyekevu Mungu atamwokoa. 30 Atamwokoa na huyo asiye na hatia; Naam, utaokolewa kwa sababu ya usafi wa mikono yako.

Ayubu 23

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Hata leo mashitaka yangu yana uchungu; Pigo langu ni zito zaidi ya kuugua kwangu. 3 Laiti ningejua mahali niwezapo kumwona, Nifike hata hapo anapokaa! 4 Ningeiweka daawa yangu mbele yake, Na kukijaza kinywa changu hoja. 5 Ningeyajua maneno atakayonijibu, Na kuelewa na hayo atakayoniambia. 6 Je! Angeshindana nami kwa ukuu wa uwezo wake? La, lakini angenisikiliza. 7 Hapo walekevu wangepata kuhojiana naye; Basi hivyo ningeachiliwa na mwamuzi wangu milele. 8 Tazama, naenda mbele, wala hayuko; Narudi nyuma, lakini siwezi kumwona; 9 Na mkono wa kushoto, afanyapo kazi, lakini siwezi kumwona; Hujificha upande wa kuume, hata nisimwone. 10 Lakini yeye aijua njia niendeayo; Akisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu. 11 Mguu wangu umeshikamana sana na hatua zake; Njia yake nimeishika, wala sikukengeuka. 12 Sikurudi nyuma kuiacha amri ya midomo yake; Nimeyatunza maneno ya kinywa chake zaidi ya riziki yangu, 13 Lakini yeye ni mmoja, ni nani awezaye kumgeuza? Tena nafsi yake ilitakalo, ndilo afanyalo. 14 Kwani yeye hulitimiliza hilo nililoamuriwa; Tena mambo mengi kama hayo ya pamoja naye. 15 Kwa hiyo naona taabu mbele ya uso wake; Nitakapofikiri, namwogopa. 16 Kwani Mungu ameufanya moyo wangu kuzimia, Naye Mwenyezi amenitaabisha; 17 Maana sikufadhaishwa kwa sababu ya giza, Wala kwa sababu giza kuu limenifunika uso.

Ayubu 24

1 Mbona nyakati zisiwekwe na Mwenyezi? Na hao wamjuao mbona hawazioni siku zake? 2 Wako waziondoao alama za mipaka; Huyachukua makundi kwa jeuri na kuyalisha. 3 Humfukuza punda wake asiye baba, Humtwaa rehani ng'ombe wake mwanamke mjane. 4 Humgeuza mhitaji aiache njia; Maskini wa nchi hujificha pamoja. 5 Tazama, kama punda-mwitu jangwani Wao hutoka kwenda kazini mwao, wakitafuta chakula kwa bidii; Jangwa huwapa chakula cha watoto wao. 6 Hukata nafaka zao mashambani; Na kuokota zabibu za waovu. 7 Hujilaza usiku kucha uchi pasipo nguo, Wala hawana cha kujifunika baridi. 8 Hutota kwa manyunyo ya milimani, Na kuambatana na jabali kwa kukosa sitara, 9 Wako wamwondoao matitini kwa nguvu huyo asiye na baba, Na kutwaa rehani kwa maskini; 10 Hata wazunguke uchi pasipo mavazi, Nao wakiwa na njaa huchukua miganda; 11 Hushindika mafuta ndani ya makuta ya watu hao; Wakanyaga mashinikizo, nao wana kiu. 12 Watu huugua toka mji ulio na watu wengi, Na roho yake aliyejeruhiwa hupiga ukelele; Wala Mungu hauangalii upumbavu. 13 Hawa ni katika hao waliouasi mwanga; Hawazijui njia zake, Wala hawakai katika mapito yake. 14 Mwuaji huamka asubuhi kukipambauka, huwaua maskini na wahitaji; Tena wakati wa usiku yu kama mwivi. 15 Tena jicho lake mzinifu hungojea wakati wa giza-giza, Akisema, Hapana jicho litakaloniona; Naye huuficha uso wake. 16 Wao hutoboa nyumba gizani; Hujifungia ndani wakati wa mchana; Hawaujui mwanga. 17 Kwani asubuhi kwao wote ni kama giza tupu; Kwani wao wavijua vitisho vya hiyo giza tupu. 18 Mwasema, Yeye ni mwepesi juu ya uso wa gharika; Sehemu yao inalaaniwa duniani; Hageuki kwenda njia ya mizabibuni. 19 Chaka na hari hukausha maji ya theluji; Kuzimu nako hao ambao wamefanya dhambi. 20 Tumbo lililomzaa litamsahau; buu litamla na kuona tamu; Hatakumbukwa tena; Na udhalimu utavunjwa kama mti. 21 Naam, yeye huwala walio tasa wasiozaa; Wala hamtendei mema mwanamke mjane. 22 Lakini Mungu huwadumisha wenye uwezo kwa nguvu zake; Huinuka, wasiokuwa na tumaini la kuishi. 23 Huwapa kuwa na salama, nao wapumzika kwayo; Na macho yake ya juu ya njia zao. 24 Wao wametukuzwa; lakini kitambo kidogo hutoweka; Naam, hushushwa, na kuondolewa njiani kama wengine wote, Nao hukatwa kama vile masuke ya ngano. 25 Na kama sivyo sasa, ni nani atakayenihukumu kuwa ni mwongo, Na kuyafanya maneno yangu kuwa si kitu?

Ayubu 25

1 Ndipo Bildadi, Mshuhi, akajibu, na kusema, 2 Enzi na hofu zi pamoja naye; Hufanya amani katika mahali pake palipoinuka. 3 Je! Majeshi yake yahesabika? Ni nani asiyetokewa na mwanga wake? 4 Basi mtu awezaje kuwa na haki mbele ya Mungu? Au awezaje kuwa safi aliyezaliwa na mwanamke? 5 Tazama, hata mwezi hauangazi, Wala nyota si safi machoni pake; 6 Siuze mtu, aliye mdudu! Na mwanadamu, ambaye ni buu!

Ayubu 26

1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, 2 Jinsi ulivyomsaidia huyo asiye na uwezo! Jinsi ulivyouokoa mkono usio na nguvu! 3 Jinsi ulivyomshauri huyo asiye na hekima! Na kutangaza ujuzi wa kweli kwa wingi! 4 Je! Umetamka maneno kwa nani? Kisha ni roho ya nani iliyotoka kwako? 5 Hao waliokufa watetema Chini ya maji na hao wayakaao. 6 Kaburi li wazi mbele yake, Uharibifu nao hauna kifuniko. 7 Yeye hutandaza kaskazi juu ya nafasi isiyo na kitu, Na kuutundika ulimwengu pasipo kitu. 8 Huyafunga maji ndani ya mawingu yake mazito; Na hilo wingu halipasuki chini yake. 9 Husitiri uso wa kiti chake cha enzi, Na kulitandaza wingu lake juu yake. 10 Amepiga duara kuwa ni mpaka juu ya uso wa maji, Hata hapo mwanga na giza vinapopakana. 11 Nguzo za mbingu zatetemeka, Na kustaajabu kwa kukemea kwake. 12 Huichafua bahari kwa uwezo wake, Na kumtema Rahabu kwa akili zake. 13 Hizo mbingu hupambwa kwa roho yake; Mkono wake umemchoma nyoka aendaye mbio. 14 Tazama, hivi ni viunga tu vya njia zake; Na jinsi yalivyo madogo manong'ono tusikiayo katika habari zake! Lakini ngurumo za uweza wake ni nani awezaye kuelewa nazo?

Ayubu 27

1 Kisha Ayubu akaendelea na mithali yake, na kusema, 2 Kama aishivyo Mungu, aliyeniondolea haki yangu; Huyo Mwenyezi aliyeitesa nafsi yangu; 3 (Kwa kuwa uhai wangu ukali mzima ndani yangu, Na roho ya Mungu i katika pua yangu;) 4 Hakika midomo yangu haitanena yasiyo haki, Wala ulimi wangu hautatamka udanganyifu. 5 Hasha! Nisiwahesabie ninyi kuwa na haki; Hata nitakapokufa sitajiondolea uelekevu wangu. 6 Haki yangu naishika sana, wala sitaiacha; Moyo wangu hautanisuta wakati nikiwapo hai. 7 Adui yangu na awe kama huyo mwovu, Na mwenye kuondoka kinyume changu na awe kama asiye haki. 8 Kwani tumaini la mpotovu ni nini, ingawa ajipatia faida, Hapo Mungu amwondoleapo roho yake? 9 Je! Mungu atakisikia kilio chake, Taabu zitakapomfikilia? 10 Je! Atajifurahisha katika Mwenyezi, Na kumlingana Mungu nyakati zote? 11 Nitawafundisha ninyi mambo ya mkono wa Mungu; Hayo yaliyo kwa Mwenyezi sitayaficha. 12 Tazama, ninyi nyote mmeyaona wenyewe; Mbona basi mmebatilika kabisa? 13 Hii ndiyo sehemu ya mtu mwovu kwa Mungu, Na urithi wa hao waoneao, waupokeao kwa Mwenyezi. 14 Watoto wake wakiongezeka ni kwa upanga; Na wazao wake hawatashiba chakula. 15 Hao watakaosalia kwake watazikwa katika kufa, Wala wajane wake waliofiwa na waume hawataomboleza. 16 Ajapokusanya fedha kama mavumbi, Na kujifanyia mavazi kama udongo kwa wingi; 17 Yumkini kuyatengeza, lakini wenye haki watayavaa, Nao wasio na hatia watazigawanya hizo fedha. 18 Yeye hujenga nyumba yake kama mdudu, Na kama kibanda afanyacho mlinzi. 19 Yeye hujilaza hali ni tajiri, lakini ndio mwisho; Hufunua macho yake, naye hayuko. 20 Vitisho vyampata kama maji mengi; Dhoruba humwiba usiku. 21 Upepo wa mashariki humchukua, naye huondoka; Na kumkumba atoke mahali pake. 22 Kwani Mungu atamtupia asimhurumie; Angependa kuukimbia mkono wake. 23 Watu watampigia makofi, Na kumzomea atoke mahali pake.

Ayubu 28

1 Hakika kuna shimo wachimbako fedha, Na mahali wapatapo dhahabu waisafishayo. 2 Chuma hufukuliwa katika ardhi, Na shaba huyeyushwa katika mawe. 3 Binadamu hukomesha giza; Huyatafuta-tafuta hata mpaka ulio mbali, Mawe ya giza kuu, giza tupu. 4 Hufukua shimo mbali na makao ya watu; Husahauliwa na nyayo zipitazo; Huning'inia mbali na watu, huyumba-yumba huko na huko. 5 Katika ardhi ndimo kitokeamo chakula; Na chini yake hupinduliwa kama kwa moto. 6 Mawe yake ni mahali zipatikanapo yakuti; Nayo ina mchanga wa dhahabu. 7 Njia ile hapana ndege mkali aijuaye, Wala jicho la tai halijaiona; 8 Wanyama wakali wajivunao hawajaikanyaga, Wala simba mkali hajaipita. 9 Huunyoshea mwamba wa gumegume mkono wake; Huipindua milima hata misingi yake. 10 Hukata mifereji kati ya majabali; Na jicho lake huona kila kito cha thamani 11 Hufunga vijito visichuruzike; Na kitu kilichostirika hukifunua. 12 Bali hekima itapatikana wapi? Na mahali pa ufahamu ni wapi? 13 Mwanadamu hajui thamani yake, Wala haionekani katika nchi ya walio hai. 14 Vilindi vyasema, Haimo ndani yangu; Na bahari yasema, Haiko kwangu. 15 Haipatikani kwa dhahabu, Wala fedha haitapimwa iwe thamani yake. 16 Haiwezi kutiwa thamani kwa dhahabu ya Ofiri, Wala kwa shohamu ya thamani nyingi, wala kwa yakuti ya samawi. 17 Dhahabu na vioo haviwezi kulinganishwa nayo; Wala kubadili kwake hakutakuwa kwa vyombo vya dhahabu safi. 18 Havitatajwa fedhaluka wala bilauri; Naam, kima cha hekima chapita marijani. 19 Yakuti ya rangi ya manjano ya Kushi haitasawazishwa nayo, Wala haitatiwa kima kwa dhahabu safi. 20 Basi hekima yatoka wapi? Na mahali pa ufahamu ni wapi? 21 Kwa kuwa imefichwa mbali na macho ya wote walio hai, Na kusitirika na ndege wa angani. 22 Uharibifu na Mauti husema, Tumesikia habari zake kwa masikio yetu. 23 Mungu ndiye aijuaye njia yake, Naye anajua mahali pake. 24 Maana anatazama hata miisho ya nchi, Na kuona chini ya mbingu nzima. 25 Apate kuufanyia upepo uzito wake; Naam, anayapima maji kwa kipimo. 26 Hapo alipoiwekea mvua amri, Na njia kwa umeme wa radi. 27 Ndipo alipoiona na kuitangaza; Aliithibitisha, naam, na kuichunguza. 28 Kisha akamwambia mwanadamu, Tazama, kumcha Bwana ndiyo hekima, Na kujitenga na uovu ndio ufahamu.

Ayubu 29

1 Kisha Ayubu akaendelea na mithali yake, na kusema, 2 Laiti ningekuwa kama nilivyokuwa katika miezi ya kale, Kama katika siku hizo Mungu aliponilinda; 3 Hapo taa yake ilipomulika juu yangu kichwani, Nami nilitembea gizani kwa njia ya mwanga wake; 4 Kama nilivyokuwa katika siku zangu za kukomaa, Hapo siri ya Mungu ilipokuwa hemani mwangu; 5 Wakati Mwenyezi alipokuwa akali pamoja nami, Nao watoto wangu walipokuwa wakinizunguka; 6 Wakati hatua zangu zilipokuwa zikioshwa kwa siagi, Nalo jabali liliponimiminia mito ya mafuta! 7 Wakati nilipotoka kwenda mjini, hata langoni, Nilipokitengeza kiti changu katika njia kuu, 8 Hao vijana waliniona wakajificha, Nao wazee wakaniondokea na kusimama; 9 Wakuu wakanyamaa wasinene, Na kuweka mikono yao vinywani mwao; 10 Sauti yao masheki ilinyamaa, Na ndimi zao zilishikamana na makaakaa yao. 11 Maana sikio liliponisikia, ndipo likanibarikia; Na jicho liliponiona, likanishuhudia. 12 Kwa sababu nalimwokoa maskini aliyenililia; Yatima naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia. 13 Baraka yake yeye aliyekuwa karibu na kupotea ilinijia; Nikaufanya moyo wa mjane kuimba kwa furaha. 14 Nalijivika haki, ikanifunika, Adili yangu ilikuwa kama joho na kilemba. 15 Nalikuwa macho kwa kipofu, Nalikuwa miguu kwa aliyechechemea. 16 Nalikuwa baba kwa mhitaji, Na daawa ya mtu nisiyemjua naliichunguza. 17 Nami nilizivunja taya za wasio haki, Na kumpokonya mawindo katika meno yake. 18 Ndipo niliposema, Nitakufa ndani ya kioto changu, Nami nitaziongeza siku zangu kama mchanga; 19 Shina langu limeenea hata kufika majini, Na umande hukaa usiku kucha katika matawi yangu; 20 Utukufu wangu utakuwa mpya kwangu, Na uta wangu hurejezwa upya mkononi mwangu. 21 Watu walitega masikio kunisikiliza, na kungoja, Wakanyamaa kimya wapate sikia mashauri yangu. 22 Hawakunena tena baada ya kusikia maneno yangu; Matamko yangu yakadondoka juu yao. 23 Walikuwa wakiningojea kama kungojea mvua; Wakafunua vinywa vyao sana kama mvua ya masika. 24 Walipokata tamaa nikacheka nao; Na mwanga wa uso wangu hawakuuangusha. 25 Niliwachagulia njia, nikakaa kama mkuu wao. Nikakaa kama mfalme katika jeshi la askari, Mfano wa awafarijiye hao waombolezao.

Ayubu 30

1 Lakini sasa hao walio wadogo wangu hunifanyia mzaha, Ambao baba zao niliwadharau hata kuwaweka na mbwa wa kundi langu. 2 Naam, uwezo wa mikono yao utanifaa nini? Watu ambao nguvu zao zimekoma. 3 Wamekonda kwa uhitaji na njaa; Huguguna nchi kavu, penye giza la ukiwa na uharibifu. 4 Hung'oa mboga ya chumvi kwenye kichaka; Na mizizi ya mretemu ni chakula chao. 5 Hufukuzwa watoke kati ya watu; Huwapigia kelele kama kumpigia mwivi. 6 Lazima hukaa katika mianya ya mabonde, Katika mashimo ya nchi na ya majabali. 7 Hulia kama punda vichakani; Hukusanyika chini ya upupu. 8 Wao ni wana wa wapumbavu, naam, watoto wa wahuni; Walifukuzwa kwa mijeledi watoke katika nchi. 9 Na sasa mimi nimekuwa wimbo wao, Naam, nimekuwa simo kwao. 10 Wao hunichukia, na kujitenga nami, Hawaachi kunitemea mate usoni. 11 Kwani ameilegeza kamba yake, na kunitesa, Wala hawajizuii tena mbele yangu. 12 Kwa mkono wangu wa kuume huinuka kundi; Huisukuma miguu yangu kando, Na kunipandishia njia zao za uharibifu. 13 Waiharibu njia yangu, Wauzidisha msiba wangu, Watu wasio na msaidizi. 14 Wanijilia kama wapitao katika ufa mpana; Katikati ya magofu wanishambulia. 15 Vitisho vimenigeukia; Huifukuza heshima yangu kama upepo; Na kufanikiwa kwangu kumepita kama wingu. 16 Sasa nafsi yangu inamwagika ndani yangu; Siku za mateso zimenishika. 17 Wakati wa usiku mifupa yangu huchomeka ndani yangu, Na maumivu yanayonitafuna hayapumziki. 18 Kwa ugonjwa wangu kuwa na nguvu nyingi Mavazi yangu yameharibika; Hunikaza kama shingo ya kanzu yangu. 19 Yeye amenibwaga topeni, Nami nimekuwa kama mavumbi na majivu. 20 Nakulilia wewe, wala huniitikii; Nasimama, nawe wanitazama tu. 21 Wewe umegeuka kuwa mkali kwangu; Nawe waniudhi kwa uweza wa mkono wako. 22 Waniinua juu hata upeponi, na kunipandisha juu yake; Nawe waniyeyusha katika dhoruba. 23 Kwani najua kuwa utanileta hata kifoni, Niifikilie nyumba waliyoandikiwa wenye uhai wote. 24 Je! Mtu katika kuanguka kwake hanyoshi mkono? Na kulilia msaada katika msiba wake? 25 Je! Mimi sikulia kwa ajili ya huyo aliyekuwa katika taabu? Nafsi yangu, je! Haikusononeka kwa ajili ya wahitaji? 26 Hapo nilipotazamia mema, ndipo yakaja mabaya; Nami nilipongojea mwanga, likaja giza. 27 Matumbo yangu yatokota, wala hayaachi; Siku za taabu zimenijilia. 28 Naenda nikiomboleza pasipo jua; Nasimama katika mkutano, na kuulilia msaada. 29 Mimi ni ndugu yao mbwa-mwitu, Ni mwenzao mbuni. 30 Ngozi yangu ni nyeusi, nayo yanitoka, Na mifupa yangu imeteketea kwa hari. 31 Kwa hiyo kinanda changu kimegeuzwa kuwa maombolezo, Na filimbi yangu kuwa sauti yao waliao.

Ayubu 31

1 Nilifanya agano na macho yangu; Basi nawezaje kumwangalia msichana? 2 Kwani sehemu ya Mungu itokayo juu ingekuwa nini, Na urithi wa Mwenyezi utokao juu? 3 Je! Siyo msiba kwa wasio haki, Na hasara kwao watendao uovu? 4 Je! Yeye hazioni njia zangu, Na kuzihesabu hatua zangu zote? 5 Kwamba nimetembea katika ubatili, Na mguu wangu umeukimbilia udanganyifu; 6 (Na nipimwe katika mizani iliyo sawasawa, Ili Mungu aujue uelekevu wangu); 7 Kwamba hatua yangu imekengeuka na kuiacha njia, Na moyo wangu kuyaandama macho yangu, Tena kwamba kipaku cho chote kimeshikamana na mikono yangu; 8 Basi na nipande, mwingine ale; Naam, mazao ya shamba langu na yang'olewe. 9 Kama moyo wangu ulishawishwa kwa mwanamke, Nami nimeotea mlangoni pa jirani yangu; 10 Ndipo hapo mke wangu na asage kwa mwingine, Na wengine na wainame juu yake. 11 Kwani hilo lingekuwa kosa kuu; Naam, lingekuwa ni uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; 12 Kwa kuwa ni moto uteketezao hata Uharibifu, Nao ungeyang'oa maongeo yangu yote. 13 Kama nimeidharau daawa ya mtumishi wangu, au ya kijakazi changu, Waliposhindana nami; 14 Basi Mungu atakapoinuka nitafanya nini? Naye atakapozuru, nitamjibuje? 15 Je! Huyo aliyenifanya mimi ndani ya tumbo, siye aliyemfanya na yeye? Si yeye mmoja aliyetufinyanga tumboni? 16 Ikiwa nimewanyima maskini haja zao, Au kama nimeyatia kiwi macho ya mwanamke mjane; 17 Au kama nimekula tonge langu peke yangu, Mayatima wasipate kulila; 18 (La, tangu ujana wangu alikua pamoja nami kama kwa baba; Nami nimekuwa ni kiongozi cha mjane tangu tumbo la mamangu); 19 Ikiwa nimemwona mtu kuangamia kwa kukosa nguo, Au wahitaji kukosa mavazi; 20 Ikiwa viuno vyake havikunibarikia, Au kama hakupata moto kwa manyoya ya kondoo zangu; 21 Ikiwa nimewainulia mayatima mkono, Nilipoona msaada wangu langoni; 22 Basi bega langu na lianguke kutoka mahali pake, Na mkono wangu uvunjike mfupani mwake. 23 Kwani msiba utokao kwa Mungu ulikuwa na kitisho kwangu, Na kwa sababu ya ukuu wake sikuweza kufanya neno. 24 Ikiwa nimeifanya dhahabu kuwa tumaini langu, Na kuiambia dhahabu safi, Wewe u tegemeo langu; 25 Kama nilifurahi kwa kuwa mali yangu yalikuwa mengi, Na kwa sababu mkono wangu umepata vitu vingi; 26 Kama nililitazama jua lilipoangaza, Au mwezi ukiendelea katika kung'aa; 27 Na moyo wangu umeshawishwa kwa siri, Na midomo yangu imeubusu mkono wangu; 28 Hilo nalo lingekuwa uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; Kwani ningemwambia uongo Mungu aliye juu. 29 Kama nilifurahi kwa kuangamia kwake huyo aliyenichukia, Au kujitukuza alipopatikana na maovu; 30 (Naam, sikukiacha kinywa changu kufanya dhambi Kwa kuutaka uhai wake kwa kuapiza); 31 Kama watu wa hemani mwangu hawakunena, Ni nani awezaye kumpata mtu asiyeshibishwa na yeye kwa nyama? 32 Mgeni hakulala njiani; Lakini nilimfungulia msafiri milango yangu; 33 Ikiwa kama mwanadamu nimeyafunika makosa yangu, Kwa kuuficha uovu wangu kifuani mwangu; 34 Kwa sababu niliwaogopa mkutano mkubwa, Na dharau la jamaa lilinitia hofu, Hata nilinyamaa kimya, nisitoke mlangoni- 35 Laiti ningekuwa na mtu wa kunisikia! (Tazama, sahihi yangu ni hii, Mwenyezi na anijibu); Laiti ningekuwa na hayo mashitaka yaliyoandikwa na adui yangu! 36 Hakika ningeyachukua mabegani; Ningejifungia mfano wa kilemba. 37 Ningemwambia hesabu ya hatua zangu Ningemkaribia kama vile mkuu. 38 Kama nchi yangu yalia juu yangu, Na matuta yake hulia pamoja; 39 Kama nimeyala matunda yake pasipo kulipa, Au kama nimewafanya wenyewe kupotewa na uhai; 40 Miiba na imee badala ya ngano, Na magugu badala ya shayiri. Maneno ya Ayubu yamekoma hapa.

Ayubu 32

1 Basi hao watu watatu wakaacha kumjibu Ayubu, kwa sababu alikuwa mwenye haki machoni pake mwenyewe. 2 Ndipo zikawaka hasira za huyo Elihu mwana wa Barakeli, Mbuzi, katika jamaa ya Ramu, juu ya Ayubu, kwa sababu alikuwa amejipa haki mwenyewe zaidi ya Mungu. 3 Tena hasira zake ziliwaka juu ya hao rafiki zake watatu kwa sababu hawakupata jawabu, lakini wamemhukumia Ayubu makosa. 4 Basi huyo Elihu alikuwa anangoja ili anene na Ayubu, kwa sababu hao wengine walikuwa wazee kuliko yeye. 5 Hata Elihu alipoona kuwa hapana jawabu katika vinywa vya watu hao watatu, hasira zake ziliwaka. 6 Basi Elihu mwana wa Barakeli, Mbuzi, akajibu, na kusema, Mimi ni kijana, na ninyi ni wazee sana; Kwa hiyo nilijizuia, nisithubutu kuwaonyesha nionavyo. 7 Nilisema, Yafaa siku ziseme, Na wingi wa miaka ufundishe hekima. 8 Lakini imo roho ndani ya mwanadamu, Na pumzi za Mwenyezi huwapa akili. 9 Sio wakuu walio wenye akili, Wala sio wazee watambuao hukumu. 10 Basi nilisema, Nisikilizeni mimi; Mimi nami nitawaonyesha nionavyo. 11 Tazama, niliyangojea maneno yenu, Nilizisikiliza nisikie hoja zenu, Hapo mlipokitafuta mtakalonena. 12 Naam, niliwasikiza ninyi, Na tazama, hapana mmoja aliyemshinda Ayubu, Wala kumjibu maneno yake, kati yenu. 13 Jitunzeni msiseme, Sisi tumepata hekima; Mungu yumkini akamshinda, si mtu; 14 Kwa kuwa yeye hajayaelekeza maneno yake kwangu; Wala sitamjibu mimi kwa maneno yenu. 15 Wameshangaa, hawajibu tena; Hawana neno la kusema. 16 Na mimi, je! Ningoje, kwa sababu hawaneni, Kwa sababu wasimama kimya, wala wasijibu tena; 17 Mimi nami nitajibu sehemu yangu, Mimi nami nitaonyesha nionavyo. 18 Kwa kuwa nimejaa maneno; Roho iliyo ndani yangu hunihimiza. 19 Tazama, tumbo langu ni kama divai iliyozibwa; Kama viriba vipya li karibu na kupasuka. 20 Nitanena, ili nipate kutulia; Nitafunua midomo yangu na kujibu. 21 Tafadhali, nisiupendelee uso wa mtu; Wala sitajipendekeza kwa mtu ye yote. 22 Kwani mimi sijui kujipendekeza; Au Muumba wangu angeniondoa kwa upesi.

Ayubu 33

1 Walakini, Ayubu, nakuomba usikilize matamko yangu, Ukayasikilize maneno yangu yote. 2 Tazama basi, nimefunua kinywa changu, Ulimi wangu umenena kinywani mwangu. 3 Maneno yangu yatatamka uelekevu wa moyo wangu; Na hayo niyajuayo midomo yangu itayanena kwa unyofu. 4 Roho ya Mungu imeniumba, Na pumzi za Mwenyezi hunipa uhai. 5 Kwamba waweza, nijibu; Yapange maneno yako sawasawa mbele yangu, usimame. 6 Tazama, mimi ni mbele ya Mungu kama ulivyo wewe; Mimi nami nilifinyangwa katika udongo. 7 Tazama, utisho wangu hautakutia hofu wewe, Wala sitakulemea kwa uzito. 8 Hakika umenena masikioni mwangu, Nami nimesikia sauti ya maneno yako, ukisema, 9 Mimi ni safi, sina makosa; Sina hatia, wala hapana uovu ndani yangu; 10 Tazama, yuaona sababu za kufarakana nami, Hunihesabu kuwa ni adui yake; 11 Hunitia miguu yangu katika mkatale, Na mapito yangu yote huyapeleleza. 12 Tazama, nitakujibu, katika neno hili huna haki; Kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mwanadamu. 13 Nawe kwani kumnung'unikia, Kwa vile asivyotoa hesabu ya mambo yake yote? 14 Kwa kuwa Mungu hunena mara moja, Naam, hata mara ya pili, ajapokuwa mtu hajali. 15 Katika ndoto, katika maono ya usiku, Usingizi mzito uwajiliapo watu, Katika usingizi kitandani; 16 Ndipo huyafunua masikio ya watu, Na kuyatia muhuri mafundisho yao, 17 Ili amwondoe mtu katika makusudio yake, Na kumfichia mtu kiburi; 18 Yeye huizuia nafsi yake isiende shimoni, Na uhai wake usiangamie kwa upanga. 19 Yeye hutiwa adabu kwa maumivu kitandani mwake, Na kwa mashindano yaendeleayo daima mifupani mwake; 20 Hata roho yake huchukia chakula, Na nafsi yake huchukia nyama nzuri. 21 Nyama ya mwili wake huliwa, isionekane; Na mifupa yake isiyoonekana yatokea nje. 22 Naam, nafsi yake inakaribia shimoni, Na uhai wake unakaribia waangamizi. 23 Kwamba akiwapo malaika pamoja naye, Mkalimani, mmoja katika elfu, Ili kumwonyesha binadamu hayo yampasayo; 24 Ndipo amwoneapo rehema, na kusema, Mwokoe asishuke shimoni; Mimi nimeuona ukombozi. 25 Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; Huzirudia siku za ujana wake; 26 Yeye humwomba Mungu, naye akamtakabalia; Hata auone uso wake kwa furaha; Naye humrejezea mtu haki yake. 27 Yeye huimba mbele ya watu, na kusema, Mimi nimefanya dhambi, na kuyapotosha hayo yaliyoelekea, Wala sikulipizwa jambo hilo; 28 Yeye ameikomboa nafsi yangu isiende shimoni, Na uhai wangu utautazama mwanga. 29 Tazama, hayo yote ni Mungu anayeyafanya, Mara mbili, naam, hata mara tatu, kwa mtu, 30 Ili kurudisha roho yake itoke shimoni, Ili atiwe mwanga kwa mwanga wa walio hai. 31 Angalia sana, Ee Ayubu, unisikilize; Nyamaza, mimi nitasema. 32 Kama una neno la kusema, nijibu; Nena, kwani nataka kukuhesabia kuwa na haki. 33 Kama sivyo, unisikilize mimi; Nyamaza, nami nitakufunza hekima.

Ayubu 34

1 Tena Elihu akajibu na kusema, 2 Sikilizeni maneno yangu, enyi wenye hekima; Tegeni masikio kwangu, ninyi mlio na maarifa. 3 Kwa kuwa sikio huyajaribu maneno, Kama vile kaakaa lionjavyo chakula. 4 Na tujichagulie yaliyo ya uelekevu; Na tujue wenyewe yaliyo mema. 5 Kwani Ayubu amesema, Mimi ni mwenye haki, Naye Mungu ameniondolea haki yangu; 6 Nijapokuwa mwenye haki, nimehesabiwa kuwa mwongo; Jeraha yangu haiponyeki, nijapokuwa sina makosa. 7 Je! Ni mtu gani mfano wa Ayubu, Anywaye mzaha kama maji? 8 Atembeaye na hao watendao uovu, Na kwenda pamoja na watu wabaya. 9 Kwa kuwa amenena, Haimfai mtu lo lote Kujifurahisha na Mungu. 10 Kwa hiyo nisikilizeni, enyi wenye fahamu; Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; Wala Mwenyezi kufanya uovu. 11 Kwani atamlipa binadamu kwa kazi yake, Naye atamfanya kila mtu kuona sawasawa na njia zake 12 Naam, hakika, Mungu hatatenda mabaya, Wala Mwenyezi hatapotosha hukumu. 13 Ni nani aliyemwagiza kuiangalia dunia? Au ni nani aliyemwekea ulimwengu huu wote? 14 Kama akimwekea mtu moyo wake, Akijikusanyia roho yake na pumzi zake; 15 Wenye mwili wote wataangamia pamoja, Nao wanadamu watarejea tena kuwa mavumbi. 16 Ikiwa una ufahamu, sikia neno hili; Isikilize sauti ya maneno yangu. 17 Je! Atatawala mtu aichukiaye haki hata mmoja? Nawe, je! Utamhukumia mkosa aliye na haki na mwenye nguvu? 18 Je! Inafaa kumwambia mfalme, Wewe u mwovu? Au kuwaambia wakuu, Ninyi ni wabaya? 19 Sembuse huyo asiyependelea nyuso za wakuu, Wala hawajali matajiri kuliko maskini? Kwani wote ni kazi ya mikono yake, 20 Hufa ghafula, hata usiku wa manane; Watu hutikisika na kwenda zao, Nao mashujaa huondolewa pasipo mkono wa mtu. 21 Kwani macho yake ya juu ya njia za mtu, Naye huiona miendo yake yote. 22 Hapana weusi, wala hilo giza tupu, Wawezapo kujificha watendao udhalimu. 23 Kwani yeye hana haja ya kumfikiria mtu zaidi, ili aende mbele za Mungu ahukumiwe. 24 Yeye huwavunja-vunja mashujaa pasina kuwachunguza, Na kuwaweka wengine mahali pao. 25 Kwa sababu hiyo yeye huyatafiti matendo yao; Naye huwapindia usiku, wakaangamia. 26 Yeye huwapiga kama watu wabaya Waziwazi mbele ya macho ya wengine; 27 Kwa sababu walikengeuka, wasimwandame yeye, Wasikubali kuzishika njia zake hata moja; 28 Hata wakafanya kilio cha maskini kumfikilia, Naye akasikia kilio cha hao wateswao. 29 Akitoa utulivu yeye, ni nani awezaye kuhukumia makosa? Akificha uso wake, ni nani awezaye kumtazama? Kama hufanyiwa taifa, au mtu mmoja, ni sawasawa; 30 Kwamba huyo mpotovu asitawale, Pasiwe na wa kuwatega watu. 31 Kwani kuna mtu aliyemwambia Mungu, Mimi nimevumilia kurudiwa, ingawa sikukosa; 32 Nisiyoyaona nifundishe wewe; Kama nimefanya uovu sitafanya tena? 33 Je! Malipo yake yatakuwa kama upendavyo wewe, hata ukayakataa? Kwani yakupasa wewe kuchagua, si mimi; Kwa sababu hiyo sema uyajuayo. 34 Watu walio na akili wataniambia, Naam, kila mtu mwenye hekima anisikiaye; 35 Huyo Ayubu amesema pasipo maarifa, Na maneno yake hayana hekima. 36 Laiti Ayubu angejaribiwa hata mwisho, Kwa kuwa amejibu kama watu waovu. 37 Kwani huongeza uasi juu ya dhambi zake, Apiga makofi kati yetu, Na kuongeza maneno yake kinyume cha Mungu.

Ayubu 35

1 Tena Elihu akajibu na kusema, 2 Je! Wewe wadhani kwamba haya ni haki yako, Au je! Wasema, Haki yangu ni zaidi kuliko ya Mungu, 3 Maana wasema, Kutakuwa na faida gani kwako wewe? Tena, Nitapata faida gani, kuliko nikifanya dhambi? 4 Mimi nitakujibu, Na hawa wenzio pamoja nawe. 5 Ziangalie mbingu ukaone; Na mawingu yaangalie, yaliyo juu kuliko wewe. 6 Ikiwa umefanya dhambi, umefanya nini juu yake? Yakiwa makosa yako yameongezeka, wamfanyia nini yeye? 7 Ikiwa u mwenye haki, wampa kitu gani? Au yeye hupokea nini mkononi mwako? 8 Uovu wako waweza kumwumiza mtu kama wewe; Na haki yako yaweza kumfaa mwanadamu. 9 Kwa sababu ya wingi wa jeuri wao hulia; Walilia msaada kwa sababu ya mkono wa wakuu. 10 Wala hapana asemaye, Yuko wapi Mungu Muumba wangu, Awapaye nyimbo wakati wa usiku; 11 Atufundishaye zaidi ya hayawani wa nchi, Na kutufanya wenye hekima kuliko ndege za angani? 12 Hulia huko, lakini hapana ajibuye, Kwa sababu ya kiburi cha watu waovu. 13 Hakika Mungu hatasikia ubatili, Wala Mwenyezi hatauangalia. 14 Sembuse usemapo wewe ya kuwa humwangalii, Hiyo daawa i mbele yake, nawe wamngojea! 15 Lakini sasa, kwa sababu yeye hakukujilia katika hasira zake, Wala hauangalii sana unyeti; 16 Ndiposa Ayubu hufunua kinywa chake kwa ubatili; Huongeza maneno pasipo maarifa.

Ayubu 36

1 Tena Elihu akaendelea na kusema, 2 Ningojee kidogo nami nitakueleza; Kwa kuwa nikali na maneno kwa ajili ya Mungu. 3 Nitayaleta maarifa yangu kutoka mbali, Nami nitampa haki Muumba wangu. 4 Kwani yakini maneno yangu si ya uongo; Aliyekamilika katika maarifa yu pamoja nawe. 5 Tazama, Mungu ni hodari, wala hamdharau mtu ye yote; Ana uweza katika nguvu za fahamu. 6 Hauhifadhi uhai wa waovu; Lakini huwapa wateswao haki yao. 7 Yeye hawaondolei macho yake wenye haki; Lakini pamoja na wafalme huwaweka Katika viti vya enzi milele, nao hutukuzwa. 8 Nao wakifungwa kwa pingu, Wakitwaliwa kwa kamba za mateso; 9 Ndipo huwaonyesha matendo yao, Na makosa yao, ya kuwa wametenda kwa kujivuna. 10 Yeye huyafunua masikio yao, wasikie maonyo, Na kuwaagiza warudi kuuacha uovu. 11 Kama wakisikia na kumtumikia, Watapisha siku zao katika kufanikiwa, Na miaka yao katika furaha. 12 Lakini wasiposikia, wataangamia kwa upanga, Nao watakufa pasipo maarifa. 13 Lakini hao wasiomcha Mungu mioyoni hujiwekea hasira Hawalilii msaada hapo awafungapo. 14 Wao hufa wakali vijana, Na uhai wao huangamia katikati ya wachafu. 15 Yeye humponya aliyetaabika kwa njia ya taabu yake, Na kuyafunua masikio yao kwa maonevu. 16 Naam, yeye angekuongoza utoke katika msiba Hata mahali penye nafasi, ambapo hapana msonge; Na kilichowekwa mezani pako kingejaa mafuta. 17 Lakini umejaa hukumu ya waovu; Hukumu na haki hukushika. 18 Basi ujitunze, isije hasira ikakuvuta hata ukafanya mzaha; Wala usikubali ukuu wa ukombozi ukugeuze. 19 Je! Mali yako yatatosha, hata usiwe katika taabu, Au uwezo wote wa nguvu zako? 20 Usiutamani usiku, Wakati watu wakatwapo katika mahali pao. 21 Jitunze, usiutazame uovu; Kwani umeuchagua huo zaidi ya taabu. 22 Tazama, Mungu hutenda makuu kwa uweza wake; Ni nani afundishaye kama yeye? 23 Ni nani aliyemwagiza njia yake? Au ni nani awezaye kusema, Wewe umetenda yasiyo haki? 24 Kumbuka kuitukuza kazi yake, Watu waliyoiimbia. 25 Wanadamu wote wameitazama; Watu huiangalia kwa mbali 26 Tazama, Mungu ni mkuu, nasi hatumjui; Hesabu ya miaka yake haitafutiki. 27 Kwani yeye huvuta juu matone ya maji, Yamwagikayo katika mvua kutoka kungeni mwake; 28 Ambayo mawingu yainyesha Na kudondoza juu ya wanadamu kwa wingi. 29 Naam, mtu aweza kuelewa na matandazo ya mawingu, Ngurumo za makao yake? 30 Tazama, yeye huutandaza mwanga wake, umzunguke; Naye hufunika vilindi vya bahari. 31 Kwani huwahukumu kabila za watu kwa njia hizi; Hutoa chakula kwa ukarimu. 32 Yeye huifunika mikono yake kwa umeme; Na kuuagiza shabaha utakayopiga. 33 Mshindo wake hutoa habari zake, Anayewaka hasira juu ya uovu.

Ayubu 37

1 Moyo wangu hunitetema kwayo pia, Nao hutoka mahali pake. 2 Zisikizeni hizo kelele za sauti yake, Na uvumi utokao kinywani mwake. 3 Yeye huituma iende chini ya mbingu zote, Na radi yake hata miisho ya nchi. 4 Baadaye sauti hunguruma; Yeye hunguruma kwa sauti ya ukuu wake; Hazizuii hapo sauti yake isikiwapo. 5 Mungu hunguruma kwa kustaajabisha kwa sauti yake; Hufanya mambo makuu, ambayo hatuwezi kuelewa nayo. 6 Kwani huiambia theluji, Anguka juu ya nchi; Na vivyo manyonyota ya mvua, Na hayo maji ya mvua yake kubwa. 7 Huufunga mkono wa kila binadamu; Ili watu wote aliowaumba wajue. 8 Hapo wanyama huingia mafichoni, Na kukaa katika mapango yao. 9 Dhoruba hutoka katika vyumba vyake; Na baridi ghalani mwake. 10 Barafu huletwa kwa pumzi za Mungu; Na upana wa maji huganda. 11 Naam, huyatweka mawingu mazito mzigo wa maji; Hulitandika wingu la umeme wake; 12 Nalo hugeuzwa huku na huku kwa uongozi wake, Ili yafanye yote atakayoyaagiza Juu ya uso wa dunia hii ikaayo watu; 13 Kama ni kwa kuonya, au kama ni kwa nchi yake, Au kama ni kwa rehema, ndiye aletaye. 14 Sikiliza neno hili, Ee Ayubu; Simama kimya, uzifikiri kazi za Mungu za ajabu. 15 Je! Wajua wewe jinsi Mungu anavyoziagiza, Na kuumulikisha umeme wa wingu lake? 16 Je! Wajua jinsi mawingu yalivyowekwa sawasawa, Hizo kazi za ajabu za huyo mkamilifu wa maarifa? 17 Jinsi nguo zako zilivyo na moto, Hapo nchi ituliapo kwa sababu ya upepo wa kusini? 18 Je! Waweza kuzitandaza mbingu pamoja naye, Ambazo zina nguvu kama kioo cha kuyeyushwa? 19 Utufundishe ni maneno gani tutakayomwambia; Kwa maana hamwezi kuyatengeza kwa sababu ya giza. 20 Je! Aambiwe kwamba nataka kunena? Au mtu angetamani kumezwa? 21 Na sasa watu hawawezi kuutazama mwanga ung'aao mbinguni; Lakini upepo ukipita huzitakasa. 22 Kaskazini hutokea umemetufu wa dhahabu; Mungu huvikwa ukuu utishao. 23 yeye Mwenyezi hamwezi kumwona; Yeye ni mkuu mwenye uweza; Tena mwenye hukumu, na mwingi wa haki, hataonea. 24 Kwa hiyo watu humwogopa; Yeye hawaangalii walio na hekima mioyoni.

Ayubu 38

1 Ndipo Bwana akamjibu Ayubu katika upepo wa kisulisuli, na kusema, 2 Ni nani huyu atiaye mashauri giza Kwa maneno yasiyo na maarifa? 3 Basi jifunge viuno kama mwanamume, Maana nitakuuliza neno, nawe niambie. 4 Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? Haya! Sema, kama ukiwa na ufahamu. 5 Ni nani aliyeamrisha vipimo vyake, kama ukijua? Au ni nani aliyenyosha kamba juu yake? 6 Misingi yake ilikazwa juu ya kitu gani? Au ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni, 7 Hapo nyota za asubuhi zilipoimba pamoja, Na wana wote wa Mungu walipopiga kelele kwa furaha? 8 Au ni nani aliyeifunga bahari kwa milango, Hapo ilipofurika kana kwamba imetoka tumboni. 9 Nilipolifanya wingu kuwa vazi lake, Na giza zito kuwa nguo ya kuifungia, 10 Nikaiagiza amri yangu; Nikaiwekea makomeo na milango, 11 Nikasema, Utafika mpaka hapa, lakini hutapita, Na hapa mawimbi yako yanyetayo yatazuiliwa? 12 Je! Umeiamuru asubuhi tangu siku zako zilipoanza? Umeyajulisha mapambazuko mahali pake? 13 Yapate kuishika miisho ya nchi, Waovu wakung'utwe wakawe mbali nayo? 14 Hubadilika mfano wa udongo chini ya muhuri, Vitu vyote vinatokea kama mavazi. 15 Na waovu nuru yao huzuiliwa isiwafikie, Na mkono ulioinuka huvunjika. 16 Je! Umeziingia chemchemi za bahari, Au umetembea mahali pa siri pa vilindi? 17 Je! Umefunuliwa malango ya mauti, Au umeyaona malango ya kuzimu? 18 Umeyafahamu mapana ya dunia? Haya! Sema, ikiwa unayajua hayo yote. 19 Iko wapi njia ya kuyafikia makao ya nuru? Na giza pia, mahali pake ni wapi? 20 Upate kuipeleka hata mpaka wake, Upate kuelewa na mapito ya kuiendea nyumba yake? 21 Hukosi unajua, maana ulizaliwa wakati huo, Na hesabu ya siku zako ni kubwa! 22 Je! Umeziingia ghala za theluji, Au umeziona ghala za mvua ya mawe, 23 Nilizoziweka akiba kwa wakati wa misiba, Kwa siku ya mapigano na vita? 24 Je! Nuru hutengwa kwa njia gani, Au upepo wa mashariki hutawanywaje juu ya nchi? 25 Ni nani aliyepasua mfereji kwa maji ya gharika, Au njia kwa umeme wa radi; 26 Kunyesha mvua juu ya nchi isiyo na watu; Juu ya jangwa asiyokaa mwanadamu; 27 Kuishibisha nchi iliyo kame na ukiwa, Na kuyameza majani yaliyo mororo? 28 Je! Mvua ina baba? Au ni nani aliyeyazaa matone ya umande? 29 Barafu ilitoka katika tumbo la nani? Na sakitu ya mbinguni ni nani aliyeizaa? 30 Maji hugandamana kama jiwe, Na uso wa vilindi huganda kwa baridi. 31 Je! Waweza kuufunga mnyororo wa Kilimia, Au kuvilegeza vifungo vya Orioni? 32 Je! Waweza kuziongoza Sayari kwa wakati wake? Au waweza kuongoza Dubu na watoto wake? 33 Je! Unazijua amri zilizoamuriwa mbingu? Waweza kuyathibitisha mamlaka yake juu ya dunia? 34 Waweza kuiinua sauti yako mpaka mawinguni, ili wingi wa maji ukufunikize? 35 Waweza kuutuma umeme, nao ukaenda, Ukakuambia, Sisi tupo hapa? 36 Je! Ni nani aliyetia hekima moyoni? Au ni nani aliyetia ufahamu rohoni? 37 Ni nani awezaye kuyahesabu mawingu kwa hekima? Au ni nani awezaye kuzimimina chupa za mbinguni? 38 Wakati mavumbi yagandamanapo, Na madongoa kushikamana pamoja? 39 Je! Utamwindia simba mke mawindo? Au utashibisha njaa ya simba wachanga, 40 Waoteapo mapangoni mwao, Wakaapo mafichoni wapate kuvizia? 41 Ni nani anayempatia kunguru chakula, Makinda yake wanapomlilia Mungu, Na kutanga-tanga kwa kutindikiwa na chakula?

Ayubu 39

1 Je! Wajua majira ya kuzaa kwao mbuzi-mwitu walio majabalini? Au waweza kusema majira ya kuzaa kulungu? 2 Je! Waweza kuhesabu miezi yao watakayoitimiza? Au je! Wajua majira ya kuzaa kwao? 3 Wao hujiinamisha, kuzaa watoto wao, Watupa taabu zao. 4 Watoto wao wa katika hali nzuri, hukua katika bara wazi; Huenda zao, wala hawarudi tena. 5 Ni nani aliyempeleka punda-milia aende huru? Au je! Ni nani aliyemfungulia vifungo punda-mwitu? 6 Ambaye nimeifanya nyika kuwa nyumba yake, Na nchi ya chumvi kuwa makao yake. 7 Yeye hudharau mshindo wa mji, Wala hasikii kelele zake msimamizi. 8 Upana wa milima ni malisho yake, Hutafuta-tafuta kila kitu kilicho kibichi. 9 Je! Nyati atakubali kukutumikia? Au atakaa katika zizi lako? 10 Je! Waweza kumfunga nyati kwa kamba matutani? Au, yeye atayalima mabonde nyuma yako? 11 Je! Utamtumaini kwa sababu ana nguvu nyingi? Au, utamwachia yeye kazi yako? 12 Je! Utamtumaini kwamba ataileta mbegu yako nyumbani. Na kukusanya nafaka ya kiwanja chako cha kupuria? 13 Bawa la mbuni hufurahi; Lakini mabawa yake na manyoya yake, je! Yana huruma? 14 Kwani yeye huyaacha mayai yake juu ya nchi, Na kuyatia moto mchangani, 15 Na kusahau kwamba yumkini mguu kuyavunja, Au mnyama wa mwitu kuyakanyaga. 16 yeye huyafanyia ukali makinda yake, kana kwamba si yake; Ijapokuwa taabu yake ni ya bure, hana hofu; 17 Kwa sababu Mungu amemnyima akili, Wala hakumpa fahamu. 18 Wakati anapojiinua juu aende, Humdharau farasi na mwenye kumpanda. 19 Je! Wewe ulimpa farasi uwezo wake? Au, ni wewe uliyemvika shingo yake manyoya yatetemayo? 20 Ndiwe uliyemfanya aruke kama nzige? Fahari ya mlio wake hutisha. 21 Hupara-para bondeni, na kuzifurahia nguvu zake; Hutoka kwenda kukutana na wenye silaha. 22 Yeye hufanyia kicho dhihaka, wala hashangai; Wala hageuki kurudi nyuma mbele ya upanga. 23 Podo humpigia makelele, Mkuki ung'aao na fumo. 24 Huimeza nchi kwa ukali wake na ghadhabu; Wala hasimami kwa sauti ya baragumu. 25 Kila ipigwapo baragumu yeye husema, Aha! Naye husikia harufu ya vita toka mbali, Mshindo wa maakida, na makelele. 26 Je! Mwewe huruka juu kwa akili zako, Na kuyanyosha mabawa yake kwenda kusini? 27 Je! Tai hupaa juu kwa amri yako, Na kufanya kioto chake mahali pa juu? 28 Hukaa jabalini, ndiko kwenye malazi yake, Juu ya genge la jabali, na ngomeni. 29 Toka huko yeye huchungulia mawindo; Macho yake huyaangalia toka mbali. 30 Makinda yake nayo hufyonza damu; Na kwenye maiti ndiko aliko.

Ayubu 40

1 Bwana akafuliza kumjibu Ayubu, na kusema, 2 Je! Mwenye hoja atashindana na Mwenyezi? Mwenye kujadiliana na Mungu, na ajibu yeye. 3 Ndipo Ayubu akamjibu Mungu, na kusema, 4 Tazama, mimi si kitu kabisa, nikujibu nini? Naweka mkono wangu kinywani pangu. 5 Nimenena mara moja, nami sitajibu; Naam, nimenena mara mbili, lakini sitaendelea zaidi. 6 Ndipo Bwana akamjibu Ayubu katika upepo wa kisulisuli, na kusema, 7 Jifunge viuno kama mwanamume, Mimi nitakuuliza neno, nawe niambie. 8 Je! Hata hukumu yangu utaibatilisha? Utanitia mimi hatiani, upate kuhesabiwa haki? 9 Au je! Wewe una mkono kama Mungu? Waweza kutoa ngurumo kwa sauti kama yeye? 10 Haya! Jivike sasa fahari na ukuu; Jipambe heshima na enzi. 11 Mwaga mafuriko ya hasira zako, Ukamtazame kila mtu mwenye kiburi, ukamdhili. 12 Mtazame kila mtu mwenye kiburi ukamshushe, Ukawakanyage waovu hapo wasimamapo. 13 Wafiche mavumbini pamoja, Wafunge nyuso zao mahali palipositirika. 14 Ndipo mimi nami nitazikiri habari zako, Ya kuwa mkono wako wa kuume waweza kukuokoa. 15 Mwangalie huyo kiboko, niliyemwumba pamoja nawe; Yeye hula nyasi kama vile ng'ombe, 16 Tazama basi, nguvu zake ni katika viuno vyake, Na uwezo wake u katika mishipa ya tumbo lake. 17 Yeye hutikisa mkia wake mfano wa mwerezi; Mishipa ya mapaja yake yanaungamana pamoja. 18 Mifupa yake ni kama mirija ya shaba; Mbavu zake ni kama vipande vya chuma. 19 Yeye ni mkuu wa njia za Mungu; Yeye aliyemfanya alimpa upanga wake. 20 Hakika milima humtolea chakula; Hapo wachezapo wanyama wote wa barani. 21 Hulala chini ya miti yenye vivuli, Mafichoni penye mianzi, na matopeni. 22 Hiyo miti yenye vivuli humfunika kwa vivuli vyao; Mierebi ya vijito humzunguka. 23 Tazama, mto ukifurika, yeye hatetemeki; Hujiona yu salama, ijapokuwa Yordani hufurika hata kinywani pake. 24 Je! Mtu ye yote atamnasa akiwa yu macho, Au, kumtoboa pua yake kwa mtego?

Ayubu 41

1 Je! Waweza wewe kumvua mamba kwa ndoana? Au, kuufunga ulimi wake kwa kamba? 2 Je! Waweza kutia kamba puani mwake? Au kutoboa taya yake kwa kulabu? 3 Je! Atakusihi sana? Au, atakuambia maneno ya upole? 4 Je! Atafanya agano pamoja nawe, Umtwae kuwa mtumishi wako milele? 5 Je! Utamchezea kama ndege? Au, kumfunga kwa ajili ya wasichana wako? 6 Je! Vikosi vya wavuvi watamfanyia biashara? Watamgawanya kati ya wafanyao biashara? 7 Je! Waweza kuijaza ngozi yake na vyuma vyenye ncha, Au kichwa chake kwa vyusa? 8 Mwekee mkono wako; Vikumbuke vile vita, wala usifanye tena. 9 Tazama, kumtamani ni bure; Je! Hatambwaga chini huyo atakayemtazama? 10 Hapana aliye mkali hata akathubutu kumwamsha; Bali ni nani awezaye kusimama mbele yangu mimi? 11 Ni nani aliyetangulia kunipa hata nimlipe? Kila kilicho chini ya mbingu nzima ni changu. 12 Sitanyamaa kusema habari za via vyake, Wala nguvu zake kuu, wala umbo lake zuri. 13 Ni nani awezaye kumbambua magamba yake? Ni nani atakayepenya dirii yake maradufu? 14 Ni nani awezaye kuifungua milango ya uso wake? Meno yake yatisha kandokando yake. 15 Magamba yake yenye nguvu ndiyo fahari yake, Yamefungamana pamoja kama kwa kufungwa kwa muhuri. 16 Jinsi yalivyoshikamana Hata upepo hauwezi kupita kati. 17 Yamefungamana pamoja; Yameshikamana, hata hayawezekani kutengwa. 18 Kwa kuchemua kwake mwanga humemetuka, Na macho yake yanafanana na makope ya alfajiri. 19 Mienge iwakayo hutoka kinywani mwake, Na macheche ya moto huruka nje. 20 Moshi hutoka katika mianzi ya pua yake, Kama nyungu ikitokota, na manyasi yawakayo. 21 Pumzi zake huwasha makaa, Na miali ya moto hutoka kinywani mwake. 22 Katika shingo yake hukaa nguvu, Na utisho hucheza mbele yake. 23 Manofu ya nyama yake hushikamana; Yanakazana juu yake; hayawezi kuondolewa. 24 Moyo wake una imara kama jiwe; Naam, imara kama jiwe la chini la kusagia. 25 Anapojiinua, mashujaa huogopa; Kwa sababu ya woga wao huvunjwa moyo. 26 Mtu akimpiga kwa upanga, haumwingii; Wala fumo, wala mshale, wala mkuki wenye ncha. 27 Yeye huona chuma kuwa kama nyasi, Na shaba kama mti uliooza. 28 Mshale hauwezi kumkimbiza; Na mawe ya teo kwake hugeuka kuwa kama makapi. 29 Marungu huhesabiwa kama mabua; Naye hucheka mshindo wa mkuki ukitupwa. 30 Pande zake za chini ni kama vigae vikali; Hutandika malazi kama kuweka chombo cha kupuria nafaka juu ya matope. 31 Yeye huchemsha kilindi mfano wa nyungu; Hufanya bahari kuwa kama mafuta. 32 Hufanya mapito yake kung'aa nyuma yake Hata mtu angedhani kilindi kina mvi. 33 Juu ya nchi hapana aliyefanana naye, Aliyeumbwa pasipo oga. 34 Yeye hutazama kila kitu kilicho juu; Ni mfalme juu ya wote wenye kiburi.

Ayubu 42

1 Ndipo Ayubu akamjibu Bwana, na kusema. 2 Najua ya kuwa waweza kufanya mambo yote, Na ya kuwa makusudi yako hayawezi kuzuilika. 3 Ni nani huyu afichaye mashauri bila maarifa? Kwa maana, nimesema maneno nisiyoyafahamu, Mambo ya ajabu ya kunishinda mimi, nisiyoyajua. 4 Sikiliza, nakusihi, nami nitanena; Nitakuuliza neno, nawe niambie. 5 Nilikuwa nimesikia habari zako, kwa kusikia kwa masikio; Bali sasa jicho langu linakuona. 6 Kwa sababu hiyo najichukia nafsi yangu, na kutubu Katika mavumbi na majivu. 7 Basi ikawa, baada ya Bwana kumwambia Ayubu maneno hayo, Bwana akamwambia huyo Elifazi Mtemani, Hasira zangu zinawaka juu yako, na juu ya hao rafiki zako wawili; kwa kuwa ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu. 8 Basi sasa, jitwalieni ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba, mkamwendee mtumishi wangu Ayubu, mjisongezee sadaka ya kuteketezwa; na huyo mtumishi wangu Ayubu atawaombea ninyi; kwa kuwa nitamridhia yeye, nisiwatende sawasawa na upumbavu wenu; kwani ninyi hamkunena maneno yaliyonyoka katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu. 9 Basi Elifazi, Mtemani, na Bildadi, Mshuhi, na Sofari, Mnaamathi, wakaenda, wakafanya kama vile Bwana alivyowaamuru; naye Bwana akamridhia Ayubu. 10 Kisha Bwana akaugeuza uteka wa Ayubu, hapo alipowaombea rafiki zake; Bwana naye akampa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza. 11 Ndipo wakamwendea nduguze wote, waume kwa wake, nao wote waliojuana naye hapo zamani, wakala chakula pamoja naye katika nyumba yake; nao wakamlilia na kumtuza moyo katika habari za huo uovu wote Bwana aliouleta juu yake; kila mtu akampa kipande cha fedha, na pete ya dhahabu kila mmoja. 12 Basi hivyo Bwana akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng'ombe elfu, na punda wake elfu. 13 Tena alikuwa na wana waume saba, na binti watatu. 14 Akamwita huyo wa kwanza jina lake Yemima; na wa pili akamwita jina lake Kesia; na wa tatu akamwita jina lake Keren-hapuhu. 15 Katika nchi hiyo yote hawakuwapo wanawake waliokuwa wazuri kama hao wana wa Ayubu; na baba yao akawapa urithi kati ya ndugu zao wana waume. 16 Kisha baada ya mambo hayo Ayubu akaishi miaka mia na arobaini, naye akawaona wanawe, na wana wa wanawe, hata vizazi vinne. 17 Basi Ayubu akafa, mzee sana mwenye kujawa na siku.

Zaburi 1

1 Heri mtu yule asiyekwenda Katika shauri la wasio haki; Wala hakusimama katika njia ya wakosaji; Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha. 2 Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo, Na sheria yake huitafakari mchana na usiku. 3 Naye atakuwa kama mti uliopandwa Kandokando ya vijito vya maji, Uzaao matunda yake kwa majira yake, Wala jani lake halinyauki; Na kila alitendalo litafanikiwa. 4 Sivyo walivyo wasio haki; Hao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo. 5 Kwa hiyo wasio haki hawatasimama hukumuni, Wala wakosaji katika kusanyiko la wenye haki. 6 Kwa kuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki, Bali njia ya wasio haki itapotea.

Zaburi 2

1 Mbona mataifa wanafanya ghasia, Na makabila wanatafakari ubatili? 2 Wafalme wa dunia wanajipanga, Na wakuu wanafanya shauri pamoja, Juu ya Bwana, Na juu ya masihi wake. 3 Na tuvipasue vifungo vyao, Na kuzitupia mbali nasi kamba zao. 4 Yeye aketiye mbinguni anacheka, Bwana anawafanyia dhihaka. 5 Ndipo atakaposema nao kwa hasira yake, Na kuwafadhaisha kwa ghadhabu yake. 6 Nami nimemweka mfalme wangu Juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu. 7 Nitaihubiri amri; Bwana aliniambia, Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa. 8 Uniombe, nami nitakupa mataifa kuwa urithi wako, Na miisho ya dunia kuwa milki yako. 9 Utawaponda kwa fimbo ya chuma, Na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi. 10 Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili, Enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe. 11 Mtumikieni Bwana kwa kicho, Shangilieni kwa kutetemeka. 12 Shikeni yaliyo bora asije akafanya hasira, Nanyi mkapotea njiani,Kwa kuwa hasira yake itawaka upesi,Heri wote wanaomkimbilia.

Zaburi 3

1 Bwana, watesi wangu wamezidi kuwa wengi, Ni wengi wanaonishambulia, 2 Ni wengi wanaoiambia nafsi yangu, Hana wokovu huyu kwa Mungu. 3 Na Wewe, Bwana, U ngao yangu pande zote, Utukufu wangu na mwinua kichwa changu. 4 Kwa sauti yangu namwita Bwana Naye aniitikia toka mlima wake mtakatifu. 5 Nalijilaza nikalala usingizi, nikaamka, Kwa kuwa Bwana ananitegemeza. 6 Sitayaogopa makumi elfu ya watu, Waliojipanga juu yangu pande zote. 7 Bwana, uinuke, Mungu wangu, uniokoe, Maana umewapiga taya adui zangu wote; Umewavunja meno wasio haki. 8 Wokovu una Bwana; Baraka yako na iwe juu ya watu wako.

Zaburi 4

1 Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo; Umenifanyizia nafasi wakati wa shida; Unifadhili na kuisikia sala yangu. 2 Enyi wanadamu, hata lini utukufu wangu utafedheheka? Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo? 3 Bali jueni ya kuwa Bwana amejiteulia mtauwa; Bwana atasikia nimwitapo. 4 Mwe na hofu wala msitende dhambi, Tafakarini vitandani mwenu na kutulia. 5 Toeni dhabihu za haki, Na kumtumaini Bwana. 6 Wengi husema, Nani atakayetuonyesha mema? Bwana, utuinulie nuru ya uso wako. 7 Umenitia furaha moyoni mwangu, Kupita yao wanapozidishiwa nafaka na divai. 8 Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, Maana Wewe, Bwana, peke yako, Ndiwe unijaliaye kukaa salama.

Zaburi 5

1 Ee Bwana, uyasikilize maneno yangu, Ukuangalie kutafakari kwangu. 2 Uisikie sauti ya kilio changu, Ee Mfalme wangu na Mungu wangu, Kwa maana Wewe ndiwe nikuombaye. 3 Bwana, asubuhi utaisikia sauti yangu, Asubuhi nitakupangia dua yangu na kutazamia. 4 Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya; Mtu mwovu hatakaa kwako; 5 Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako; Unawachukia wote watendao ubatili. 6 Utawaharibu wasemao uongo; Bwana humzira mwuaji na mwenye hila 7 Bali mimi, kwa wingi wa fadhili zako, Nitaingia nyumbani mwako; Na kusujudu kwa kicho, Nikilielekea hekalu lako takatifu. 8 Bwana, uniongoze kwa haki yako, Kwa sababu yao wanaoniotea. Uisawazishe njia yako mbele ya uso wangu, 9 Maana vinywani mwao hamna uaminifu; Mtima wao ni shimo tupu, koo lao ni kaburi wazi, Ulimi wao hujipendekeza. 10 Wewe, Mungu, uwapatilize, Na waanguke kwa mashauri yao. Uwatoe nje kwa ajili ya wingi wa makosa yao, Kwa maana wamekuasi Wewe. 11 Nao wote wanaokukimbilia watafurahi; Watapiga daima kelele za furaha. Kwa kuwa Wewe unawahifadhi, Walipendao jina lako watakufurahia. 12 Kwa maana Wewe utambariki mwenye haki; Bwana, utamzungushia radhi kama ngao.

Zaburi 6

1 Bwana, usinikemee kwa hasira yako, Wala usinirudi kwa ghadhabu yako. 2 Bwana, unifadhili, maana ninanyauka; Bwana, uniponye, mifupa yangu imefadhaika. 3 Na nafsi yangu imefadhaika sana; Na Wewe, Bwana, hata lini? 4 Bwana urudi, uniopoe nafsi yangu, Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako. 5 Maana mautini hapana kumbukumbu lako; Katika kuzimu ni nani atakayekushukuru? 6 Nimechoka kwa kuugua kwangu; Kila usiku nakieleza kitanda changu; Nalilowesha godoro langu kwa machozi yangu. 7 Jicho langu limeharibika kwa masumbufu, Na kuchakaa kwa sababu yao wanaoniudhi. 8 Ondokeni kwangu, ninyi nyote mtendao uovu; Kwa kuwa Bwana ameisikia sauti ya kilio changu. 9 Bwana ameisikia dua yangu; Bwana atayatakabali maombi yangu. 10 Adui zangu wote wataaibika na kufadhaika, Watarudi nyuma, kwa ghafula wataaibika.

Zaburi 7

1 Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe, Uniokoe na wote wanaonifuatia, uniponye. 2 Asije akaipapura nafsi yangu kama simba, Akiivunja-vunja pasipokuwa na wa kuponya. 3 Bwana, Mungu wangu, ikiwa nimetenda haya, Ikiwa mna uovu mikononi mwangu, 4 Ikiwa nimemlipa mabaya Yeye aliyekaa kwangu salama; (Hasha! Nimemponya yeye Aliyekuwa mtesi wangu bila sababu;) 5 Basi adui na anifuatie, Na kuikamata nafsi yangu; Naam, aukanyage uzima wangu, Na kuulaza utukufu wangu mavumbini. 6 Bwana uondoke kwa hasira yako; Ujiinue juu ya jeuri ya watesi wangu; Uamke kwa ajili yangu; Umeamuru hukumu. 7 Kusanyiko la mataifa na likuzunguke, Na juu yake uketi utawale. 8 Bwana atawaamua mataifa, Bwana, unihukumu mimi, Kwa kadiri ya haki yangu, Sawasawa na unyofu nilio nao. 9 Ubaya wao wasio haki na ukome, Lakini umthibitishe mwenye haki. Kwa maana mjaribu mioyo na viuno Ndiye Mungu aliye mwenye haki. 10 Ngao yangu ina Mungu, Awaokoaye wanyofu wa moyo. 11 Mungu ni mwamuzi mwenye haki, Naam, Mungu aghadhibikaye kila siku. 12 Mtu asiporejea ataunoa upanga wake; Ameupinda uta wake na kuuweka tayari; 13 Naye amemtengenezea silaha za kufisha, Akifanya mishale yake kuwa ya moto. 14 Tazama, huyu ana utungu wa uovu, Amechukua mimba ya madhara, amezaa uongo. 15 Amechimba shimo, amelichimba chini sana, Akatumbukia katika handaki aliyoifanya! 16 Madhara yake yatamrejea kichwani pake, Na dhuluma yake itamshukia utosini. 17 Nitamshukuru Bwana kwa kadiri ya haki yake; Nitaliimbia jina la Bwana aliye juu.

Zaburi 8

1 Wewe, MUNGU, Bwana wetu Jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani mwote! Wewe umeuweka utukufu wako mbinguni; 2 Vinywani mwa watoto wachanga na wanyonyao Umeiweka misingi ya nguvu; Kwa sababu yao wanaoshindana nawe; Uwakomeshe adui na mijilipiza kisasi. 3 Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, Mwezi na nyota ulizoziratibisha; 4 Mtu ni kitu gani hata umkumbuke, Na binadamu hata umwangalie? 5 Umemfanya mdogo punde kuliko Mungu; Umemvika taji ya utukufu na heshima; 6 Umemtawaza juu ya kazi za mikono yako; Umevitia vitu vyote chini ya miguu yake. 7 Kondoo, na ng'ombe wote pia; Naam, na wanyama wa kondeni; 8 Ndege wa angani, na samaki wa baharini; Na kila kipitacho njia za baharini. 9 Wewe, MUNGU, Bwana wetu, Jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani mwote!

Zaburi 9

1 Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote; Nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu; 2 Nitafurahi na kukushangilia Wewe; Nitaliimbia jina lako, Wewe Uliye juu. 3 Kwa sababu adui zangu hurudi nyuma; Hujikwaa na kuangamia mbele zako. 4 Kwa maana umenifanyia hukumu na haki Umeketi kitini pa enzi ukihukumu kwa haki. 5 Umewakemea mataifa; Na kumwangamiza mdhalimu; Umelifuta jina lao milele na milele; 6 Adui wamekoma na kuachwa ukiwa milele. Nayo miji yao uliing'oa; Hata kumbukumbu lao limepotea. 7 Bali Bwana atakaa milele, Ameweka kiti chake tayari kwa hukumu. 8 Naye atauhukumu ulimwengu kwa haki; Atawaamua watu kwa adili. 9 Bwana atakuwa ngome kwake aliyeonewa, Naam, ngome kwa nyakati za shida. 10 Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe, Maana Wewe, Bwana hukuwaacha wakutafutao. 11 Mwimbieni Bwana akaaye Sayuni, Yatangazeni kati ya watu matendo yake. 12 Maana mlipiza kisasi cha damu awakumbuka, Hakukisahau kilio cha wanyonge. 13 Wewe, Bwana, unifadhili, Tazama mateso niteswayo na wanaonichukia; Wewe uniinuaye katika malango ya mauti, 14 Ili nizisimulie sifa zako zote; Katika malango ya binti Sayuni Nitaufurahia wokovu wako. 15 Mataifa wamezama katika shimo walilolifanya; Kwa wavu waliouficha imenaswa miguu yao. 16 Bwana amejidhihirisha na kutekeleza hukumu; Amemnasa mdhalimu kwa kazi ya mikono yake. 17 Wadhalimu watarejea kuzimu, Naam, mataifa yote wanaomsahau Mungu. 18 Kwa maana mhitaji hatasahauliwa daima; Matumaini ya wanyonge hayatapotea milele. 19 Bwana, usimame, mwanadamu asipate nguvu, Mataifa wahukumiwe mbele zako. 20 Bwana, uwawekee kitisho, Mataifa na wajijue kuwa ni binadamu.

Zaburi 10

1 Ee Bwana, kwa nini wasimama mbali? Kwani kujificha nyakati za shida? 2 Kwa kiburi chake asiye haki mnyonge anafuatiwa kwa ukali; Na wanaswe kwa hila zizo hizo walizoziwaza. 3 Maana mdhalimu hujisifia tamaa ya nafsi yake, Na mwenye choyo humkana Bwana na kumdharau. 4 Mdhalimu kwa kiburi cha uso wake Asema, Hatapatiliza. Jumla ya mawazo yake ni, Hakuna Mungu; 5 Njia zake ni thabiti kila wakati. Hukumu zako ziko juu asizione, Adui zake wote awafyonya. 6 Asema moyoni mwake, Sitaondoshwa, Kizazi baada ya kizazi sitakuwamo taabuni. 7 Kinywa chake kimejaa laana, Na hila na dhuluma. Chini ya ulimi wake kuna madhara na uovu, 8 Hukaa katika maoteo ya vijiji. Mahali pa siri humwua asiye na hatia, Macho yake humvizia mtu duni. 9 Huotea faraghani kama simba pangoni, Huotea amkamate mtu mnyonge. Naam, humkamata mtu mnyonge, Akimkokota wavuni mwake. 10 Hujikunyata na kuinama; Watu duni huanguka kwa nguvu zake. 11 Asema moyoni mwake, Mungu amesahau, Auficha uso wake, haoni kamwe. 12 Bwana, uondoke, Ee Mungu, uuinue mkono wako, Usiwasahau wanyonge. 13 Kwani mdhalimu kumdharau Mungu. Akisema moyoni mwake, Hutapatiliza? 14 Umeona, maana unaangalia madhara na jeuri, Uyatwae mkononi mwako. Mtu duni hukuachia nafsi yake, Maana umekuwa msaidizi wa yatima. 15 Uuvunje mkono wake mdhalimu, Na mbaya, uipatilize dhuluma yake, hata usiione. 16 Bwana ndiye Mfalme milele na milele; Mataifa wamepotea kutoka nchi yake. 17 Bwana, umeisikia tamaa ya wanyonge, Utaitengeneza mioyo yao, utalitega sikio lako. 18 Ili kumhukumu yatima naye aliyeonewa, Binadamu aliye udongo asizidi kudhulumu.

Zaburi 11

1 Bwana ndiye niliyemkimbilia. Mbona mnaiambia nafsi yangu, Kimbia kama ndege mlimani kwenu? 2 Maana, tazama, wasio haki wanaupinda uta, Wanaitia mishale yao katika upote, Ili kuwapiga gizani wanyofu wa moyo. 3 Kama misingi ikiharibika, Mwenye haki atafanya nini? 4 Bwana yu katika hekalu lake takatifu. Bwana ambaye kiti chake kiko mbinguni, Macho yake yanaangalia; Kope zake zinawajaribu wanadamu. 5 Bwana humjaribu mwenye haki; Bali nafsi yake humchukia asiye haki, Na mwenye kupenda udhalimu. 6 Awanyeshee wasio haki mitego, Moto na kiberiti na upepo wa hari, Na viwe fungu la kikombe chao. 7 Kwa kuwa Bwana ndiye mwenye haki, Apenda matendo ya haki, Wanyofu wa moyo watamwona uso wake.

Zaburi 12

1 Bwana, uokoe, maana mcha Mungu amekoma, Maana waaminifu wametoweka katika wanadamu. 2 Husemezana yasiyofaa kila mtu na mwenziwe, Wenye midomo ya kujipendekeza; Husemezana kwa mioyo ya unafiki; 3 Bwana ataikata midomo yote ya kujipendekeza, Nao ulimi unenao maneno ya kiburi; 4 Waliosema, Kwa ndimi zetu tutashinda; Midomo yetu ni yetu wenyewe, Ni nani aliye bwana juu yetu? 5 Kwa ajili ya kuonewa kwao wanyonge, Kwa ajili ya kuugua kwao wahitaji, Sasa nitasimama, asema Bwana, Nitamweka salama yeye wanayemfyonya. 6 Maneno ya Bwana ni maneno safi, Ni fedha iliyojaribiwa kalibuni juu ya nchi; Iliyosafishwa mara saba. 7 Wewe, Bwana, ndiwe utakayetuhifadhi, Utatulinda na kizazi hiki milele. 8 Wasio haki hutembea pande zote, Ufisadi ukitukuka kati ya wanadamu.

Zaburi 13

1 Ee Bwana, hata lini utanisahau, hata milele? Hata lini utanificha uso wako? 2 Hata lini nifanye mashauri nafsini mwangu, Nikihuzunika moyoni mchana kutwa? Hata lini adui yangu atukuke juu yangu? 3 Ee Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije nikalala usingizi wa mauti. 4 Adui yangu asije akasema, Nimemshinda; Watesi wangu wasifurahi ninapoondoshwa. 5 Nami nimezitumainia fadhili zako; Moyo wangu na uufurahie wokovu wako. 6 Naam, nimwimbie Bwana, Kwa kuwa amenitendea kwa ukarimu.

Zaburi 14

1 Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, Hakuna atendaye mema. 2 Toka mbinguni Bwana aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu. 3 Wote wamepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja. 4 Je! Wote wafanyao maovu hawajui? Walao watu wangu kama walavyo mkate, Hawamwiti Bwana. 5 Hapo ndipo walipoingiwa na hofu nyingi, Maana Mungu yupo pamoja na kizazi cha haki. 6 Mnalitia aibu shauri la mtu mnyonge, Bali Bwana ndiye aliye kimbilio lake. 7 Laiti wokovu wa Israeli utoke katika Sayuni! Bwana awarudishapo wafungwa wa watu wake; Yakobo atashangilia, Israeli atafurahi.

Zaburi 15

1 Bwana, ni nani atakayekaa Katika hema yako? Ni nani atakayefanya maskani yake Katika kilima chako kitakatifu? 2 Ni mtu aendaye kwa ukamilifu, Na kutenda haki. Asemaye kweli kwa moyo wake, 3 Asiyesingizia kwa ulimi wake. Wala hakumtenda mwenziwe mabaya, Wala hakumsengenya jirani yake. 4 Machoni pake mtu asiyefaa hudharauliwa, Bali huwaheshimu wamchao Bwana Ingawa ameapa kwa hasara yake, Hayabadili maneno yake. 5 Hakutoa fedha yake apate kula riba, Hakutwaa rushwa amwangamize asiye na hatia. Mtu atendaye mambo hayo Hataondoshwa milele.

Zaburi 16

1 Mungu, unihifadhi mimi, Kwa maana nakukimbilia Wewe. 2 Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu; Sina wema ila utokao kwako. 3 Watakatifu waliopo duniani ndio Walio bora, Hao ndio niliopendezwa nao. 4 Huzuni zao zitaongezeka Wambadilio Mungu kwa mwingine; Sitazimimina sadaka zao za damu, Wala kuyataja majina yao midomoni mwangu. 5 Bwana ndiye fungu la posho langu, Na la kikombe changu; Wewe unaishika kura yangu. 6 Kamba zangu zimeniangukia mahali pema, Naam, nimepata urithi mzuri. 7 Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri, Naam, mtima wangu umenifundisha usiku. 8 Nimemweka Bwana mbele yangu daima, Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa. 9 Kwa hiyo moyo wangu unafurahi, Nao utukufu wangu unashangilia, Naam, mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini. 10 Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu, Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. 11 Utanijulisha njia ya uzima; Mbele za uso wako ziko furaha tele; Na katika mkono wako wa kuume Mna mema ya milele.

Zaburi 17

1 Ee Bwana, usikie haki, ukisikilize kilio changu, Utege sikio lako kwa maombi yangu, Yasiyotoka katika midomo ya hila. 2 Hukumu yangu na itoke kwako, Macho yako na yatazame mambo ya adili. 3 Umenijaribu moyo wangu, umenijilia usiku, Umenihakikisha usione neno; Nimenuia kinywa changu kisikose, 4 Mintarafu matendo ya wanadamu; Kwa neno la midomo yako Nimejiepusha na njia za wenye jeuri. 5 Nyayo zangu zimeshikamana na njia zako, Hatua zangu hazikuondoshwa. 6 Ee Mungu, nimekuita kwa maana utaitika, Utege sikio lako ulisikie neno langu. 7 Dhihirisha fadhili zako za ajabu Wewe uwaokoaye wanaokukimbilia; Kwa mkono wako wa kuume Uwaokoe nao wanaowaondokea. 8 Unilinde kama mboni ya jicho, Unifiche chini ya uvuli wa mbawa zako; 9 Wasinione wasio haki wanaonionea, Adui za roho yangu wanaonizunguka. 10 Wameukaza moyo wako, Kwa vinywa vyao hutoa majivuno. 11 Sasa wametuzunguka hatua zetu, Na kuyakaza macho yao watuangushe chini. 12 Kama mfano wa simba atakaye kurarua, Kama mwana-simba aoteaye katika maoteo yake. 13 Ee Bwana, usimame, umkabili, umwinamishe, Kwa upanga wako uniokoe nafsi na mtu mbaya. 14 Ee Bwana, kwa mkono wako uniokoe na watu, Watu wa dunia hii ambao fungu lao li katika maisha haya. Matumbo yao wayajaza kwa hazina yako, Hushiba wana, huwaachia watoto wao akiba zao, 15 Bali mimi nikutazame uso wako katika haki, Niamkapo nishibishwe kwa sura yako.

Zaburi 18

1 Wewe, Bwana, nguvu zangu, nakupenda sana; 2 Bwana ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia, Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu. 3 Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa, Hivyo nitaokoka na adui zangu. 4 Kamba za mauti zilinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu. 5 Kamba za kuzimu zilinizunguka, Mitego ya mauti ikanikabili. 6 Katika shida yangu nalimwita Bwana, Na kumlalamikia Mungu wangu. Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake, Kilio changu kikaingia masikioni mwake. 7 Ndipo nchi iliyotikisika na kutetemeka, Misingi ya milima ikasuka-suka; Ikatikisika kwa sababu alikuwa na ghadhabu. 8 Kukapanda moshi kutoka puani mwake, Moto ukatoka kinywani mwake ukala, Makaa yakawashwa nao. 9 Aliziinamisha mbingu akashuka, Kukawa na giza kuu chini ya miguu yake. 10 Akapanda juu ya kerubi akaruka, Naam, aliruka upesi juu ya mabawa ya upepo. 11 Alifanya giza kuwa mahali pake pa kujificha, Kuwa hema yake ya kumzunguka. Giza la maji na mawingu makuu ya mbinguni. 12 Toka mwangaza uliokuwa mbele zake Kukapita mawingu yake makuu. Mvua ya mawe na makaa ya moto. 13 Bwana alipiga radi mbinguni, Yeye Aliye juu akaitoa sauti yake, Mvua ya mawe na makaa ya moto. 14 Akaipiga mishale yake akawatawanya, Naam, umeme mwingi sana, akawatapanya. 15 Ndipo ilipoonekana mikondo ya maji, Misingi ya ulimwengu ikafichuliwa, Ee Bwana, kwa kukemea kwako, Kwa mvumo wa pumzi ya puani mwako. 16 Alipeleka kutoka juu akanishika, Na kunitoa katika maji mengi. 17 Akaniokoa na adui yangu mwenye nguvu, Na wale walionichukia, Maana walikuwa na nguvu kuliko mimi. 18 Walinikabili siku ya msiba wangu, Lakini Bwana alikuwa tegemeo langu. 19 Akanitoa akanipeleka panapo nafasi, Aliniponya kwa kuwa alipendezwa nami. 20 Bwana alinitendea sawasawa na haki yangu, Sawasawa na usafi wa mikono yangu akanilipa. 21 Maana nimezishika njia za Bwana, Wala sikumwasi Mungu wangu. 22 Hukumu zake zote zilikuwa mbele yangu, Wala amri zake sikujiepusha nazo. 23 Nami nalikuwa mkamilifu mbele zake, Nikajilinda na uovu wangu. 24 Mradi Bwana amenilipa sawasawa na haki yangu, Sawasawa na usafi wa mikono yangu mbele zake. 25 Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili; Kwa mkamilifu utajionyesha kuwa mkamilifu; 26 Kwake ajitakasaye utajionyesha kuwa mtakatifu; Na kwa mpotovu utajionyesha kuwa mkaidi. 27 Maana Wewe utawaokoa watu wanaoonewa, Na macho ya kiburi utayadhili. 28 Kwa kuwa Wewe unaiwasha taa yangu; Bwana Mungu wangu aniangazia giza langu. 29 Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi, Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta. 30 Mungu, njia yake ni kamilifu, Ahadi ya Bwana imehakikishwa, Yeye ndiye ngao yao. Wote wanaomkimbilia. 31 Maana ni nani aliye Mungu ila Bwana? Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu? 32 Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu. 33 Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu, Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. 34 Ananifundisha mikono yangu vita, Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba. 35 Nawe umenipa ngao ya wokovu wako, Mkono wako wa kuume umenitegemeza, Na unyenyekevu wako umenikuza. 36 Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Na miguu yangu haikuteleza. 37 Nitawafuatia adui zangu na kuwapata, Wala sitarudi nyuma hata wakomeshwe. 38 Nitawapiga-piga wasiweze kusimama, Wataanguka chini ya miguu yangu. 39 Nawe hunifunga mshipi wa nguvu kwa vita, Hunitiishia chini yangu walioniondokea. 40 Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Nao walionichukia nimewakatilia mbali. 41 Walipiga yowe, lakini hakuna wa kuokoa, Walimwita Bwana lakini hakuwajibu, 42 Nikawaponda kama mavumbi mbele ya upepo, Nikawatupa nje kama matope ya njiani. 43 Umeniokoa na mashindano ya watu, Umenifanya niwe kichwa cha mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. 44 Kwa kusikia tu habari zangu, Mara wakanitii. Wageni walinijia wakinyenyekea. 45 Wageni nao walitepetea, Walitoka katika ngome zao wakitetemeka. 46 Bwana ndiye aliye hai; Na ahimidiwe mwamba wangu; Na atukuzwe Mungu wa wokovu wangu; 47 Ndiye Mungu anipatiaye kisasi; Na kuwatiisha watu chini yangu. 48 Huniponya na adui zangu; Naam, waniinua juu yao walioniinukia, Na kuniponya na mtu wa jeuri. 49 Basi, Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa, Nami nitaliimbia jina lako. 50 Ampa mfalme wake wokovu mkuu, Amfanyia fadhili masihi wake,Daudi na mzao wake hata milele.

Zaburi 19

1 Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, Na anga laitangaza kazi ya mikono yake. 2 Mchana husemezana na mchana, Usiku hutolea usiku maarifa. 3 Hakuna lugha wala maneno, Sauti yao haisikilikani. 4 Sauti yao imeenea duniani mwote, Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. Katika hizo ameliwekea jua hema, 5 Kama bwana arusi akitoka chumbani mwake, Lafurahi kama mtu aliye hodari Kwenda mbio katika njia yake. 6 Kutoka kwake lautoka mwisho wa mbingu, Na kuzunguka kwake hata miisho yake, Wala kwa hari yake Hakuna kitu kilichositirika. 7 Sheria ya Bwana ni kamilifu, Huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa Bwana ni amini, Humtia mjinga hekima. 8 Maagizo ya Bwana ni ya adili, Huufurahisha moyo. Amri ya Bwana ni safi, Huyatia macho nuru. 9 Kicho cha Bwana ni kitakatifu, Kinadumu milele. Hukumu za Bwana ni kweli, Zina haki kabisa. 10 Ni za kutamanika kuliko dhahabu, Kuliko wingi wa dhahabu safi. Nazo ni tamu kuliko asali, Kuliko sega la asali. 11 Tena mtumishi wako huonywa kwazo, Katika kuzishika kuna thawabu nyingi. 12 Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake? Unitakase na mambo ya siri. 13 Umzuie mtumishi wako asitende mambo ya kiburi, Yasinitawale mimi. Ndipo nitakapokuwa kamili, Nami nitakuwa safi, sina kosa lililo kubwa. 14 Maneno ya kinywa changu, Na mawazo ya moyo wangu, Yapate kibali mbele zako, Ee Bwana, Mwamba wangu, na mwokozi wangu.

Zaburi 20

1 Bwana akujibu siku ya dhiki, Jina la Mungu wa Yakobo likuinue. 2 Akupelekee msaada toka patakatifu pake, Na kukutegemeza toka Sayuni. 3 Azikumbuke sadaka zako zote, Na kuzitakabali dhabihu zako. 4 Akujalie kwa kadiri ya haja ya moyo wako, Na kuyatimiza mashauri yako yote. 5 Na tuushangilie wokovu wako, Kwa jina la Mungu wetu tuzitweke bendera zetu. Bwana akutimizie matakwa yako yote. 6 Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake;Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu. 7 Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu. 8 Wao wameinama na kuanguka, Bali sisi tumeinuka na kusimama. 9 Bwana, umwokoe mfalme, Utuitikie siku tuitayo.

Zaburi 21

1 Ee Bwana, mfalme atazifurahia nguvu zako, Na wokovu wako ataufanyia shangwe nyingi sana. 2 Umempa haja ya moyo wake, Wala hukumzuilia matakwa ya midomo yake. 3 Maana umemsogezea baraka za heri, Umemvika taji ya dhahabu safi kichwani pake. 4 Alikuomba uhai, ukampa, Muda mrefu wa siku nyingi, milele na milele. 5 Utukufu wake ni mkuu kwa wokovu wako, Heshima na adhama waweka juu yake. 6 Maana umemfanya kuwa baraka za milele, Wamfurahisha kwa furaha ya uso wako. 7 Kwa kuwa mfalme humtumaini Bwana, Na kwa fadhili zake Aliye juu hataondoshwa. 8 Mkono wako utawapata adui zako wote, Mkono wako wa kuume utawapata wanaokuchukia. 9 Utawafanya kuwa kama tanuru ya moto, Wakati wa ghadhabu yako. Bwana atawameza kwa ghadhabu yake, Na moto utawala. 10 Matunda yao utayaharibu na kuyaondoa katika nchi, Na wazao wao katika wanadamu. 11 Madhali walinuia kukutenda mabaya, Waliwaza hila wasipate kuitimiza. 12 Kwa maana utawafanya kukupa kisogo, Kwa upote wa uta wako ukiwaelekezea mishale. 13 Ee Bwana, utukuzwe kwa nguvu zako, Nasi tutaimba na kuuhimidi uweza wako.

Zaburi 22

1 Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu? 2 Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati raha. 3 Na Wewe U Mtakatifu, Uketiye juu ya sifa za Israeli. 4 Baba zetu walikutumaini Wewe, Walitumaini, na Wewe ukawaokoa. 5 Walikulilia Wewe wakaokoka, Walikutumaini wasiaibike. 6 Lakini mimi ni mdudu wala si mtu, Laumu ya wanadamu na mzaha wa watu. 7 Wote wanionao hunicheka sana, Hunifyonya, wakitikisa vichwa vyao; 8 Husema, Umtegemee Bwana; na amponye; Na amwokoe sasa, maana apendezwa naye. 9 Naam, Wewe ndiwe uliyenitoa tumboni, Ulinitumainisha matitini mwa mama yangu. 10 Kwako nalitupwa tangu tumboni, Toka tumboni mwa mamangu ndiwe Mungu wangu. 11 Usiwe mbali nami maana taabu i karibu, Kwa maana hakuna msaidizi. 12 Mafahali wengi wamenizunguka, Walio hodari wa Bashani wamenisonga; 13 Wananifumbulia vinywa vyao, Kama simba apapuraye na kunguruma. 14 Nimemwagika kama maji, Mifupa yangu yote imeteguka, Moyo wangu umekuwa kama nta, Na kuyeyuka ndani ya mtima wangu. 15 Nguvu zangu zimekauka kama gae, Ulimi wangu waambatana na taya zangu; Unaniweka katika mavumbi ya mauti 16 Kwa maana mbwa wamenizunguka; Kusanyiko la waovu wamenisonga; Wamenizua mikono na miguu. 17 Naweza kuihesabu mifupa yangu yote; Wao wananitazama na kunikodolea macho. 18 Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura. 19 Nawe, Bwana, usiwe mbali, Ee Nguvu zangu, fanya haraka kunisaidia. 20 Uniponye nafsi yangu na upanga, Mpenzi wangu na nguvu za mbwa. 21 Kinywani mwa simba uniokoe; Naam, toka pembe za nyati umenijibu. 22 Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu, Katikati ya kusanyiko nitakusifu. 23 Ninyi mnaomcha Bwana, msifuni, Enyi nyote mlio wazao wa Yakobo, mtukuzeni, Mcheni, enyi nyote mlio wazao wa Israeli. 24 Maana hakulidharau teso la mteswa, Wala hakuchukizwa nalo; Wala hakumficha uso wake, Bali alipomlilia akamsikia. 25 Kwako zinatoka sifa zangu Katika kusanyiko kubwa. Nitaziondoa nadhiri zangu Mbele yao wamchao. 26 Wapole watakula na kushiba, Wamtafutao Bwana watamsifu; Mioyo yenu na iishi milele. 27 Miisho yote ya dunia itakumbuka, Na watu watamrejea Bwana; Jamaa zote za mataifa watamsujudia. 28 Maana ufalme una Bwana, Naye ndiye awatawalaye mataifa. 29 Wakwasi wote wa dunia watakula na kusujudu, Humwinamia wote washukao mavumbini; Naam, yeye asiyeweza kujihuisha nafsi yake, 30 Wazao wake watamtumikia. Zitasimuliwa habari za Bwana, Kwa kizazi kitakachokuja, 31 Nao watawahubiri watakaozaliwa haki yake, Ya kwamba ndiye aliyeyafanya.

Zaburi 23

1 Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. 2 Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza. 3 Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake. 4 Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. 5 Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika. 6 Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.

Zaburi 24

1 Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake. 2 Maana ameiweka misingi yake juu ya bahari, Na juu ya mito ya maji aliithibitisha. 3 Ni nani atakayepanda katika mlima wa Bwana? Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake? 4 Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, Asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili, Wala hakuapa kwa hila. 5 Atapokea baraka kwa Bwana, Na haki kwa Mungu wa wokovu wake. 6 Hiki ndicho kizazi cha wamtafutao, Wakutafutao uso wako, Ee Mungu wa Yakobo. 7 Inueni vichwa vyenu, enyi malango, Inukeni, enyi malango ya milele, Mfalme wa utukufu apate kuingia. 8 Ni nani Mfalme wa utukufu? Bwana mwenye nguvu, hodari, Bwana hodari wa vita. 9 Inueni vichwa vyenu, enyi malango, Naam, viinueni, enyi malango ya milele, Mfalme wa utukufu apate kuingia. 10 Ni nani huyu Mfalme wa utukufu? Bwana wa majeshi, Yeye ndiye Mfalme wa utukufu.

Zaburi 25

1 Ee Bwana, nakuinulia nafsi yangu, 2 Ee Mungu wangu, Nimekutumaini Wewe, nisiaibike, Adui zangu wasifurahi kwa kunishinda. 3 Naam, wakungojao hawataaibika hata mmoja; Wataaibika watendao uhaini bila sababu. 4 Ee Bwana, unijulishe njia zako, Unifundishe mapito yako, 5 Uniongoze katika kweli yako, Na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu, Nakungoja Wewe mchana kutwa. 6 Ee Bwana, kumbuka rehema zako na fadhili zako, Maana zimekuwako tokea zamani. 7 Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu, Wala maasi yangu. Unikumbuke kwa kadiri ya fadhili zako, Ee Bwana kwa ajili ya wema wako. 8 Bwana yu mwema, mwenye adili, Kwa hiyo atawafundisha wenye dhambi njia. 9 Wenye upole atawaongoza katika hukumu, Wenye upole atawafundisha njia yake. 10 Njia zote za Bwana ni fadhili na kweli, Kwao walishikao agano lake na shuhuda zake. 11 Ee Bwana, kwa ajili ya jina lako, Unisamehe uovu wangu, maana ni mwingi. 12 Ni nani amchaye Bwana? Atamfundisha katika njia anayoichagua. 13 Nafsi yake itakaa hali ya kufanikiwa; Wazao wake watairithi nchi. 14 Siri ya Bwana iko kwao wamchao, Naye atawajulisha agano lake. 15 Macho yangu humwelekea Bwana daima, Naye atanitoa miguu yangu katika wavu. 16 Uniangalie na kunifadhili, Maana mimi ni mkiwa na mteswa. 17 Katika shida za moyo wangu unifanyie nafasi, Na kunitoa katika dhiki zangu. 18 Utazame teso langu na taabu yangu; Unisamehe dhambi zangu zote. 19 Uwatazame adui zangu, maana ni wengi, Wananichukia kwa machukio ya ukali. 20 Unilinde nafsi yangu na kuniponya, Nisiaibike, maana nakukimbilia Wewe. 21 Ukamilifu na unyofu zinihifadhi, Maana nakungoja Wewe. 22 Ee Mungu, umkomboe Israeli, Katika taabu zake zote.

Zaburi 26

1 Ee Bwana, unihukumu mimi, Maana nimekwenda kwa ukamilifu wangu, Nami nimemtumaini Bwana bila wasiwasi. 2 Ee Bwana, unijaribu na kunipima; Unisafishe mtima wangu na moyo wangu. 3 Maana fadhili zako zi mbele ya macho yangu, Nami nimekwenda katika kweli yako. 4 Sikuketi pamoja na watu wa ubatili, Wala sitaingia mnamo wanafiki. 5 Nimelichukia kusanyiko la watenda mabaya, Wala sitaketi pamoja na watu waovu. 6 Nitanawa mikono yangu kwa kutokuwa na hatia, Na kuizunguka madhabahu yako, Ee Bwana 7 Ili niitangaze sauti ya kushukuru, Na kuzisimulia kazi zako za ajabu. 8 Bwana, nimependa makao ya nyumba yako, Na mahali pa maskani ya utukufu wako. 9 Usiiondoe nafsi yangu pamoja na wakosaji, Wala uhai wangu pamoja na watu wa damu. 10 Mikononi mwao mna madhara, Na mkono wao wa kuume umejaa rushwa. 11 Ila mimi nitakwenda kwa ukamilifu wangu; Unikomboe, unifanyie fadhili. 12 Mguu wangu umesimama palipo sawa; Katika makusanyiko nitamhimidi Bwana.

Zaburi 27

1 Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? 2 Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. 3 Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. 4 Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake. 5 Mradi atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, Atanisitiri katika sitara ya hema yake, Na kuniinua juu ya mwamba. 6 Na sasa kichwa changu kitainuka Juu ya adui zangu wanaonizunguka. Nami nitatoa dhabihu za shangwe hemani mwake; Nitaimba, naam, nitamhimidi Bwana. 7 Ee Bwana, usikie, kwa sauti yangu ninalia, Unifadhili, unijibu. 8 Uliposema, Nitafuteni uso wangu, Moyo wangu umekuambia, Bwana, uso wako nitautafuta. 9 Usinifiche uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu, usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu. 10 Baba yangu na mama yangu wameniacha, Bali Bwana atanikaribisha kwake. 11 Ee Bwana, unifundishe njia yako, Na kuniongoza katika njia iliyonyoka; Kwa sababu yao wanaoniotea; 12 Usinitie katika nia ya watesi wangu; Maana mashahidi wa uongo wameniondokea, Nao watoao jeuri kama pumzi. 13 Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana Katika nchi ya walio hai. 14 Umngoje Bwana, uwe hodari, Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana.

Zaburi 28

1 Ee Bwana, nitakuita Wewe, mwamba wangu, Usiwe kwangu kama kiziwi. Nisije nikafanana nao washukao shimoni, Ikiwa umeninyamalia. 2 Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo, Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu. 3 Usinikokote pamoja na wasio haki, Wala pamoja na watenda maovu. Wawaambiao jirani zao maneno ya amani, Lakini mioyoni mwao mna madhara. 4 Uwape sawasawa na vitendo vyao, Na kwa kadiri ya ubaya wa kufanya kwao, Uwape sawasawa na kazi ya mikono yao, Uwalipe stahili zao. 5 Maana hawazifahamu kazi za Bwana, Wala matendo ya mikono yake. Atawavunja wala hatawajenga; 6 Na ahimidiwe Bwana. Maana ameisikia sauti ya dua yangu; 7 Bwana ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemtumaini, Nami nimesaidiwa; Basi, moyo wangu unashangilia, Na kwa wimbo wangu nitamshukuru. 8 Bwana ni nguvu za watu wake, Naye ni ngome ya wokovu kwa masihi wake. 9 Uwaokoe watu wako, uubariki urithi wako, Uwachunge, uwachukue milele.

Zaburi 29

1 Mpeni Bwana, enyi wana wa Mungu, Mpeni Bwana utukufu na nguvu; 2 Mpeni Bwana utukufu wa jina lake; Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu. 3 Sauti ya Bwana i juu ya maji; Mungu wa utukufu alipiga radi; Bwana yu juu ya maji mengi. 4 Sauti ya Bwana ina nguvu; Sauti ya Bwana ina adhama; 5 Sauti ya Bwana yaivunja mierezi; Naam, Bwana aivunja-vunja mierezi ya Lebanoni; 6 Airusha-rusha kama ndama wa ng'ombe; Lebanoni na Sirioni kama mwana-nyati. 7 Sauti ya Bwana yaipasua miali ya moto; 8 Sauti ya Bwana yalitetemesha jangwa; Bwana alitetemesha jangwa la Kadeshi. 9 Sauti ya Bwana yawazalisha ayala, Na kuifichua misitu; Na ndani ya hekalu lake Wanasema wote, Utukufu. 10 Bwana aliketi juu ya Gharika; Naam, Bwana ameketi hali ya mfalme milele. 11 Bwana atawapa watu wake nguvu; Bwana atawabariki watu wake kwa amani.

Zaburi 30

1 Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua, Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu. 2 Ee Bwana, Mungu wangu, Nalikulilia ukaniponya. 3 Umeniinua nafsi yangu, Ee Bwana, kutoka kuzimu. Umenihuisha na kunitoa Miongoni mwao washukao shimoni. 4 Mwimbieni Bwana zaburi, Enyi watauwa wake. Na kufanya shukrani. Kwa kumbukumbu la utakatifu wake. 5 Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo, Katika radhi yake mna uhai. Huenda kilio huja kukaa usiku, Lakini asubuhi huwa furaha. 6 Nami nilipofanikiwa nalisema, Sitaondoshwa milele. 7 Bwana, kwa radhi yako Wewe uliuimarisha mlima wangu. Uliuficha uso wako, Nami nikafadhaika. 8 Ee Bwana, nalikulilia Wewe, Naam, kwa Bwana naliomba dua. 9 Mna faida gani katika damu yangu Nishukapo shimoni? Mavumbi yatakusifu? Yataitangaza kweli yako? 10 Ee Bwana, usikie, unirehemu, Bwana, uwe msaidizi wangu. 11 Uligeuza matanga yangu kuwa machezo; Ulinivua gunia, ukanivika furaha. 12 Ili utukufu wangu ukusifu, Wala usinyamaze. Ee Bwana, Mungu wangu, Nitakushukuru milele.

Zaburi 31

1 Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele. Kwa haki yako uniponye, 2 Unitegee sikio lako, uniokoe hima. Uwe kwangu mwamba wa nguvu, Nyumba yenye maboma ya kuniokoa. 3 Ndiwe genge langu na ngome yangu; Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge. 4 Utanitoa katika wavu walionitegea kwa siri, Maana Wewe ndiwe ngome yangu. 5 Mikononi mwako naiweka roho yangu; Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli. 6 Nawachukia wao washikao yasiyofaa yenye uongo; Bali mimi namtumaini Bwana. 7 Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako, Kwa kuwa umeyaona mateso yangu. Umeijua nafsi yangu taabuni, 8 Wala hukunitia mikononi mwa adui; Miguu yangu umeisimamisha panapo nafasi. 9 Ee Bwana, unifadhili, maana ni katika dhiki, Jicho langu limenyauka kwa masumbufu, Naam, mwili wangu na nafsi yangu. 10 Maana maisha yangu yamekoma kwa huzuni, Na miaka yangu kwa kuugua. Nguvu zangu zinatetemeka kwa uovu wangu, Na mifupa yangu imekauka. 11 Kwa sababu ya watesi wangu nimekuwa laumu, Naam, hasa kwa jirani zangu; Na kitu cha kutisha kwa rafiki zangu; Walioniona njiani walinikimbia. 12 Nimesahauliwa kama mfu asiyekumbukwa; Nimekuwa kama chombo kilichovunjika. 13 Maana nimesikia masingizio ya wengi; Hofu ziko pande zote. Waliposhauriana juu yangu, Walifanya hila wauondoe uhai wangu. 14 Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana, Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu. 15 Nyakati zangu zimo mikononi mwako; Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia. 16 Umwangaze mtumishi wako Kwa nuru ya uso wako; Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako. 17 Ee Bwana, nisiaibishwe, maana nimekuita; Waaibishwe wasio haki, wanyamaze kuzimuni. 18 Midomo ya uongo iwe na ububu, Imneneayo mwenye haki maneno ya kiburi, Kwa majivuno na dharau. 19 Jinsi zilivyo nyingi fadhili zako Ulizowawekea wakuchao; Ulizowatendea wakukimbiliao Mbele ya wanadamu! 20 Utawasitiri na fitina za watu Katika sitara ya kuwapo kwako; Utawaficha katika hema Na mashindano ya ndimi. 21 Bwana ahimidiwe; kwa maana amenitendea Fadhili za ajabu katika mji wenye boma. 22 Nami nalisema kwa haraka yangu, Nimekatiliwa mbali na macho yako; Lakini ulisikia sauti ya dua yangu Wakati nilipokulilia. 23 Mpendeni Bwana, Ninyi nyote mlio watauwa wake. Bwana huwahifadhi waaminifu, Humlipa atendaye kiburi malipo tele. 24 Iweni hodari, mpige moyo konde, Ninyi nyote mnaomngoja Bwana.

Zaburi 32

1 Heri aliyesamehewa dhambi, Na kusitiriwa makosa yake. 2 Heri Bwana asiyemhesabia upotovu, Ambaye rohoni mwake hamna hila. 3 Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa Kwa kuugua kwangu mchana kutwa. 4 Kwa maana mchana na usiku Mkono wako ulinilemea. Jasho langu likakauka hata nikawa Kama nchi kavu wakati wa kaskazi. 5 Nalikujulisha dhambi yangu, Wala sikuuficha upotovu wangu. Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa Bwana, Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu. 6 Kwa hiyo kila mtu mtauwa Akuombe wakati unapopatikana. Hakika maji makuu yafurikapo, Hayatamfikia yeye. 7 Ndiwe sitara yangu, utanihifadhi na mateso, Utanizungusha nyimbo za wokovu. 8 Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; Nitakushauri, jicho langu likikutazama. 9 Msiwe kama farasi wala nyumbu, Walio hawana akili. Kwa matandiko ya lijamu na hatamu Sharti kuwazuia hao, au hawatakukaribia. 10 Naye mtu mwovu ana mapigo mengi, Bali amtumainiye Bwana fadhili zitamzunguka. 11 Mfurahieni Bwana; Shangilieni, enyi wenye haki Pigeni vigelegele vya furaha; Ninyi nyote mlio wanyofu wa moyo.

Zaburi 33

1 Mpigieni Bwana vigelegele, enyi wenye haki, Kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo. 2 Mshukuruni Bwana kwa kinubi, Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa. 3 Mwimbieni wimbo mpya, Pigeni kwa ustadi kwa sauti ya shangwe. 4 Kwa kuwa neno la Bwana lina adili, Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu. 5 Huzipenda haki na hukumu, Nchi imejaa fadhili za Bwana. 6 Kwa neno la Bwana mbingu zilifanyika, Na jeshi lake lote kwa pumzi ya kinywa chake. 7 Hukusanya maji ya bahari chungu chungu, Huviweka vilindi katika ghala. 8 Nchi yote na imwogope Bwana, Wote wakaao duniani na wamche. 9 Maana Yeye alisema, ikawa; Na Yeye aliamuru, ikasimama. 10 Bwana huyabatilisha mashauri ya mataifa, Huyatangua makusudi ya watu. 11 Shauri la Bwana lasimama milele, Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi. 12 Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao, Watu aliowachagua kuwa urithi wake. 13 Toka mbinguni Bwana huchungulia, Huwatazama wanadamu wote pia. 14 Toka mahali pake aketipo Huwaangalia wote wakaao duniani. 15 yeye aiumbaye mioyo yao wote Huzifikiri kazi zao zote. 16 Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, Wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu. 17 Farasi hafai kitu kwa wokovu, Wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake. 18 Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao, Wazingojeao fadhili zake. 19 Yeye huwaponya nafsi zao na mauti, Na kuwahuisha wakati wa njaa. 20 Nafsi zetu zinamngoja Bwana; Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu. 21 Maana mioyo yetu itamfurahia, Kwa kuwa tumelitumainia jina lake takatifu. 22 Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi, Kama vile tulivyokungoja Wewe.

Zaburi 34

1 Nitamhimidi Bwana kila wakati, Sifa zake zi kinywani mwangu daima. 2 Katika Bwana nafsi yangu itajisifu, Wanyenyekevu wasikie wakafurahi. 3 Mtukuzeni Bwana pamoja nami, Na tuliadhimishe jina lake pamoja. 4 Nalimtafuta Bwana akanijibu, Akaniponya na hofu zangu zote. 5 Wakamwelekea macho wakatiwa nuru, Wala nyuso zao hazitaona haya. 6 Maskini huyu aliita, Bwana akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote. 7 Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. 8 Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini. 9 Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu. 10 Wana-simba hutindikiwa, huona njaa; Bali wamtafutao Bwana hawatahitaji kitu cho chote kilicho chema. 11 Njoni, enyi wana, mnisikilize, Nami nitawafundisha kumcha Bwana. 12 Ni nani mtu yule apendezwaye na uzima, Apendaye siku nyingi apate kuona mema? 13 Uuzuie ulimi wako na mabaya, Na midomo yako na kusema hila. 14 Uache mabaya ukatende mema, Utafute amani ukaifuatie. 15 Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao. 16 Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani. 17 Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote. 18 Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa. 19 Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote. 20 Huihifadhi mifupa yake yote, Haukuvunjika hata mmoja. 21 Uovu utamwua asiye haki, Nao wamchukiao mwenye haki watahukumiwa. 22 Bwana huzikomboa nafsi za watumishi wake, Wala hawatahukumiwa wote wamkimbiliao.

Zaburi 35

1 Ee Bwana, utete nao wanaoteta nami, Upigane nao wanaopigana nami. 2 Uishike ngao na kigao, Usimame unisaidie. 3 Uutoe na mkuki uwapinge wanaonifuatia, Uiambie nafsi yangu, Mimi ni wokovu wako. 4 Waaibishwe, wafedheheshwe, Wanaoitafuta nafsi yangu. Warudishwe nyuma, wafadhaishwe, Wanaonizulia mabaya. 5 Wawe kama makapi mbele ya upepo, Malaika wa Bwana akiwaangusha chini. 6 Njia yao na iwe giza na utelezi, Malaika wa Bwana akiwafuatia. 7 Maana bila sababu wamenifichia wavu, Bila sababu wameichimbia shimo nafsi yangu. 8 Uharibifu na umpate kwa ghafula, Na wavu aliouficha umnase yeye mwenyewe; Kwa uharibifu aanguke ndani yake. 9 Na nafsi yangu itamfurahia Bwana, Na kuushangilia wokovu wake. 10 Mifupa yangu yote itasema, Bwana, ni nani aliye kama Wewe? Umponyaye maskini na mtu aliye hodari kumshinda yeye, Naam, maskini na mhitaji na mtu amtekaye. 11 Mashahidi wa udhalimu wanasimama, Wananiuliza mambo nisiyoyajua. 12 Wananilipa mabaya badala ya mema, Hata nafsi yangu ikaingia ukiwa. 13 Bali mimi, walipougua wao, Nguo yangu ilikuwa gunia. Nalijitesa nafsi yangu kwa kufunga; Maombi yangu yakarejea kifuani mwangu. 14 Nalijifanya kama kwamba ni rafiki au ndugu yangu, Naliinama nikilia kama aliyefiwa na mamaye. 15 Lakini nikijikwaa hufurahi na kukusanyana, Walinikusanyikia watu ovyo nisiowajua, Wananipapura wala hawakomi. 16 Kama wenye mzaha wakikufuru karamuni Wananisagia meno. 17 Bwana, hata lini utatazama? Uiokoe nafsi yangu na maharabu yao, Na mpenzi wangu na wana-simba. 18 Nitakushukuru katika kusanyiko kubwa; Nitakusifu kati ya watu wengi. 19 Walio adui zangu bure wasinisimange, Wanaonichukia bila sababu wasining'ong'e. 20 Maana hawasemi maneno ya amani, Na juu ya watulivu wa nchi huwaza hila. 21 Nao wananifumbulia vinywa vyao, Husema, Ewe! Ewe! Jicho letu limeona. 22 Wewe, Bwana, umeona, usinyamaze; Ee Bwana, usiwe mbali nami. 23 Uamke, uwe macho ili kunipatia hukumu Kwa ajili ya madai yangu, Mungu wangu na Bwana wangu. 24 Unihukumu kwa haki yako, Ee Bwana, Mungu wangu, Wala wasinisimangize. 25 Wasiseme moyoni, Haya! Ndivyo tutakavyo; Wasiseme, Tumemmeza. 26 Waaibishwe, wafedheheshwe pamoja, Wanaoifurahia hali yangu mbaya. Wavikwe aibu na fedheha, Wanaojikuza juu yangu. 27 Washangilie na kufurahi, Wapendezwao na haki yangu. Naam, waseme daima, Atukuzwe Bwana, Apendezwaye na amani ya mtumishi wake. 28 Na ulimi wangu utanena haki yako, Na sifa zako mchana kutwa.

Zaburi 36

1 Kuasi kwake yule mwovu hunena moyoni mwake, Hakuna hofu ya Mungu mbele ya macho yake. 2 Kwa maana hujipendekeza machoni pake Kuwa upotovu wake hautaonekana na kuchukiwa. 3 Maneno ya kinywa chake ni uovu na hila, Ameacha kuwa na akili na kutenda mema. 4 Huwaza maovu kitandani pake, Hujiweka katika njia mbaya; ubaya hauchukii. 5 Ee Bwana, fadhili zako zafika hata mbinguni, Uaminifu wako hata mawinguni. 6 Haki yako ni kama milima ya Mungu, Hukumu zako ni vilindi vikuu, Ee Bwana, unawaokoa wanadamu na wanyama. 7 Ee Mungu, jinsi zilivyo na thamani fadhili zako! Wanadamu huukimbilia uvuli wa mbawa zako. 8 Watashibishwa kwa unono wa nyumba yako, Nawe utawanywesha mto wa furaha zako. 9 Maana kwako Wewe iko chemchemi ya uzima, Katika nuru yako tutaona nuru. 10 Uwadumishie wakujuao fadhili zako, Na wanyofu wa moyo uaminifu wako. 11 Mguu wa kiburi usinikaribie, Wala mkono wa wasio haki usinifukuze. 12 Huko ndiko walikoanguka wafanyao maovu; Wameangushwa chini wasiweze kusimama.

Zaburi 37

1 Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya, Usiwahusudu wafanyao ubatili. 2 Maana kama majani watakatika mara, Kama miche mibichi watanyauka. 3 Umtumaini Bwana ukatende mema, Ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu. 4 Nawe utajifurahisha kwa Bwana, Naye atakupa haja za moyo wako. 5 Umkabidhi Bwana njia yako, Pia umtumaini, naye atafanya. 6 Ataitokeza haki yako kama nuru, Na hukumu yako kama adhuhuri. 7 Ukae kimya mbele za Bwana, Nawe umngojee kwa saburi; Usimkasirikie yeye afanikiwaye katika njia yake, Wala mtu afanyaye hila. 8 Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, Usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya. 9 Maana watenda mabaya wataharibiwa, Bali wamngojao Bwana ndio watakaoirithi nchi. 10 Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, Utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. 11 Bali wenye upole watairithi nchi, Watajifurahisha kwa wingi wa amani. 12 Asiye haki hunuia mabaya juu ya mwenye haki, Na kumsagia meno yake. 13 Bwana atamcheka, Maana ameona kwamba siku yake inakuja. 14 Wasio haki wamefuta upanga na kupinda uta, Wamwangushe chini maskini na mhitaji, Na kuwaua wenye mwenendo wa unyofu. 15 Upanga wao utaingia mioyoni mwao wenyewe, Na nyuta zao zitavunjika. 16 Kidogo alicho nacho mwenye haki ni bora Kuliko wingi wa mali wa wasio haki wengi. 17 Maana mikono ya wasio haki itavunjika, Bali Bwana huwategemeza wenye haki. 18 Bwana anazijua siku za wakamilifu, Na urithi wao utakuwa wa milele. 19 Hawataaibika wakati wa ubaya, Na siku za njaa watashiba. 20 Bali wasio haki watapotea, Nao wamchukiao Bwana watatoweka, Kama uzuri wa mashamba, Kama moshi watatoweka. 21 Asiye haki hukopa wala halipi, Bali mwenye haki hufadhili, hukirimu. 22 Maana waliobarikiwa na yeye watairithi nchi, Nao waliolaaniwa na yeye wataharibiwa. 23 Hatua za mtu zaimarishwa na Bwana, Naye aipenda njia yake. 24 Ajapojikwaa hataanguka chini, Bwana humshika mkono na kumtegemeza. 25 Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, Lakini sijamwona mwenye haki ameachwa Wala mzao wake akiomba chakula. 26 Mchana kutwa hufadhili na kukopesha, Na mzao wake hubarikiwa. 27 Jiepue na uovu, utende mema, Na kukaa hata milele. 28 Kwa kuwa Bwana hupenda haki, Wala hawaachi watauwa wake. Wao hulindwa milele, Bali mzao wa wasio haki ataharibiwa. 29 Wenye haki watairithi nchi, Nao watakaa humo milele. 30 Kinywa chake mwenye haki hunena hekima, Na ulimi wake husema hukumu. 31 Sheria ya Mungu wake imo moyoni mwake. Hatua zake hazitelezi. 32 Mtu asiye haki humvizia mwenye haki, Na kutafuta jinsi ya kumfisha. 33 Bwana hatamwacha mkononi mwake, Wala hatamlaumu atakapohukumiwa. 34 Wewe umngoje Bwana, Uishike njia yake, Naye atakutukuza uirithi nchi, Wasio haki watakapoharibiwa utawaona. 35 Nimemwona mtu asiye haki mkali sana, Akijieneza kama mwerezi wa Lebanoni. 36 Nikapita na kumbe! Hayuko, Nikamtafuta wala hakuonekana. 37 Umwangalie sana mtu mkamilifu, Umtazame mtu mnyofu, Maana mwisho wake mtu huyo ni amani. 38 Wakosaji wataangamizwa pamoja, Wasio haki mwisho wao wataharibiwa. 39 Na wokovu wa wenye haki una Bwana; Yeye ni ngome yao wakati wa taabu. 40 Naye Bwana huwasaidia na kuwaopoa; Huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa; Kwa kuwa wamemtumaini Yeye.

Zaburi 38

1 Ee Bwana, usinilaumu katika ghadhabu yako, Wala usiniadhibu kwa ukali wa hasira yako. 2 Kwa maana mishale yako imenichoma, Na mkono wako umenipata. 3 Hamna uzima katika mwili wangu Kwa sababu ya ghadhabu yako. Wala hamna amani mifupani mwangu Kwa sababu ya hatia zangu. 4 Maana dhambi zangu zimenifunikiza kichwa, Kama mzigo mzito zimenilemea mno. 5 Jeraha zangu zinanuka, zimeoza, Kwa sababu ya upumbavu wangu. 6 Nimepindika na kuinama sana, Mchana kutwa nimekwenda nikihuzunika. 7 Maana viuno vyangu vimejaa homa, Wala hamna uzima katika mwili wangu. 8 Nimedhoofika na kuchubuka sana, Nimeugua kwa fadhaa ya moyo wangu. 9 Bwana, haja zangu zote ziko mbele zako, Kuugua kwangu hakukusitirika kwako. 10 Moyo wangu unapwita-pwita, Nguvu zangu zimeniacha; Nuru ya macho yangu nayo imeniondoka. 11 Wanipendao na rafiki zangu wanasimama mbali na pigo langu; Naam, karibu zangu wamesimama mbali. 12 Nao wanaoutafuta uhai wangu hutega mitego; Nao wanaotaka kunidhuru hunena mabaya; Na kufikiri hila mchana kutwa. 13 Lakini kama kiziwi sisikii, Nami ni kama bubu asiyefumbua kinywa chake. 14 Naam, nimekuwa kama mtu asiyesikia, Ambaye hamna hoja kinywani mwake. 15 Kwa kuwa nakungoja Wewe, Bwana, Wewe utajibu, Ee Bwana, Mungu wangu. 16 Maana nalisema, Wasije wakanifurahia; Mguu wangu ukiteleza wajitukuza juu yangu. 17 Kwa maana mimi ni karibu na kusita, Na maumivu yangu yako mbele yangu daima. 18 Kwa maana nitaungama uovu wangu, Na kusikitika kwa dhambi zangu. 19 Lakini adui zangu ni wazima wenye nguvu, Nao wanaonichukia bure wamekuwa wengi. 20 Naam, wakilipa mabaya kwa mema, Huwa adui zangu kwa kuwa nalifuata lililo jema. 21 Wewe, Bwana, usiniache, Mungu wangu, usijitenge nami. 22 Ufanye haraka kunisaidia, Ee Bwana, wokovu wangu.

Zaburi 39

1 Nalisema, Nitazitunza njia zangu Nisije nikakosa kwa ulimi wangu; Nitajitia lijamu kinywani, Maadamu mtu mbaya yupo mbele yangu. 2 Nalikuwa sisemi, nalinyamaa kimya, Sina faraja, maumivu yangu yakazidi. 3 Moyo wangu ukawa moto ndani yangu, Na katika kuwaza kwangu moto ukawaka; Nalisema kwa ulimi wangu, 4 Bwana, unijulishe mwisho wangu, Na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani; Nijue jinsi nilivyo dhaifu. 5 Tazama, umefanya siku zangu kuwa mashubiri; Maisha yangu ni kama si kitu mbele zako. Kila mwanadamu, ingawa amesitawi, ni ubatili. 6 Binadamu huenda tu huko na huko kama kivuli; Hufanya ghasia tu kwa ajili ya ubatili; Huweka akiba wala hajui ni nani atakayeichukua. 7 Na sasa ninangoja nini, Ee Bwana? Matumaini yangu ni kwako. 8 Uniokoe na maasi yangu yote, Usinifanye laumu ya mpumbavu. 9 Nimenyamaza, sitafumbua kinywa changu, Maana Wewe ndiwe uliyeyafanya. 10 Uniondolee pigo lako; Kwa uadui wa mkono wako nimeangamia. 11 Ukimrudi mtu kwa kumkemea kwa uovu wake, Watowesha uzuri wake kama nondo. Kila mwanadamu ni ubatili. 12 Ee Bwana, usikie maombi yangu, Utege sikio lako niliapo, Usiyanyamalie machozi yangu. Kwa maana mimi ni mgeni wako, Msafiri kama baba zangu wote. 13 Uniachilie nikunjuke uso, Kabla sijaondoka nisiwepo tena.

Zaburi 40

1 Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. 2 Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. 3 Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana 4 Heri aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake, Wala hakuwaelekea wenye kiburi, Wala hao wanaogeukia uongo. 5 Ee Bwana, Mungu wangu, umefanya kwa wingi Miujiza yako na mawazo yako kwetu; Hakuna awezaye kufananishwa nawe; Kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri, Ni mengi sana hayahesabiki. 6 Dhabihu na matoleo hukupendezwa nazo, Masikio yangu umeyazibua, Kafara na sadaka za dhambi hukuzitaka. 7 Ndipo niliposema, Tazama nimekuja, (Katika gombo la chuo nimeandikiwa,) 8 Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; Naam, sheria yako imo moyoni mwangu. 9 Nimehubiri habari za haki katika kusanyiko kubwa. Sikuizuia midomo yangu; Ee Bwana, unajua. 10 Sikusitiri haki yako moyoni mwangu; Nimetangaza uaminifu wako na wokovu wako. Sikuficha fadhili zako wala kweli yako Katika kusanyiko kubwa. 11 Nawe, Bwana, usinizuilie rehema zako, Fadhili zako na kweli yako na zinihifadhi daima. 12 Kwa maana mabaya yasiyohesabika Yamenizunguka mimi. Maovu yangu yamenipata, Wala siwezi kuona. Yamezidi kuliko nywele za kichwa changu, Na moyo wangu umeniacha. 13 Ee Bwana, uwe radhi kuniokoa, Ee Bwana, unisaidie hima. 14 Waaibike, wafedheheke pamoja, Wanaoitafuta nafsi yangu waiangamize. Warudishwe nyuma, watahayarishwe, Wapendezwao na shari yangu. 15 Wakae hali ya ukiwa, na iwe aibu yao, Wanaoniambia, Ewe! Ewe! 16 Washangilie, wakufurahie, Wote wakutafutao. Waupendao wokovu wako Waseme daima, Atukuzwe Bwana. 17 Nami ni maskini na mhitaji, Bwana atanitunza. Ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu, Ee Mungu wangu, usikawie.

Zaburi 41

1 Heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu. 2 Bwana atamlinda na kumhifadhi hai, Naye atafanikiwa katika nchi; Wala usimtie katika hali wamtakiayo adui zake. 3 Bwana atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia. 4 Nami nalisema, Bwana, unifadhili, Uniponye roho yangu maana nimekutenda dhambi. 5 Adui zangu wananitaja kwa maneno mabaya, Atakufa lini, jina lake likapotea? 6 Na mmoja wao akija kunitazama asema uongo, Moyo wake hujikusanyia maovu, Naye atokapo nje huyanena. 7 Wote wanaonichukia wananinong'ona, Wananiwazia mabaya. 8 Neno la kisirani limemgandama, Na iwapo amelala hatasimama tena. 9 Msiri wangu tena niliyemtumaini, Aliyekula chakula changu, Ameniinulia kisigino chake. 10 Lakini Wewe, Bwana, unifadhili, Uniinue nipate kuwalipa. 11 Kwa neno hili nimejua ya kuwa wapendezwa nami, Kwa kuwa adui yangu hasimangi kwa kunishinda. 12 Nami katika ukamilifu wangu umenitegemeza, Umeniweka mbele za uso wako milele. 13 Na atukuzwe Bwana, Mungu wa Israeli, Tangu milele hata milele. Amina na Amina.

Zaburi 42

1 Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. 2 Nafsi yangu inamwonea kiu MUNGU, Mungu aliye hai, Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? 3 Machozi yangu yamekuwa chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako. 4 Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu. 5 Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu. 6 Nafsi yangu imeinama ndani yangu, kwa hiyo nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka kilima cha Mizari. 7 Kilindi chapigia kelele kilindi kwa sauti ya maboromoko ya maji yako, Gharika zako zote na mawimbi yako yote yamepita juu yangu. 8 Mchana Bwana ataagiza fadhili zake, na usiku wimbo wake utakuwa nami, Naam, maombi kwa Mungu aliye uhai wangu. 9 Nitamwambia Mungu, mwamba wangu, Kwa nini umenisahau? Kwa nini ninakwenda nikihuzunika, adui wakinionea? 10 Watesi wangu hunitukana mithili ya kuniponda mifupa yangu, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako? 11 Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.

Zaburi 43

1 Ee Bwana, unihukumu, unitetee kwa taifa lisilo haki, Uniokoe na mtu wa hila asiye haki. 2 Kwa kuwa Wewe ndiwe Mungu uliye nguvu zangu; kwa nini umenitupa? Kwa nini ninakwenda nikihuzunika, adui wakinionea? 3 Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze, Zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako. 4 Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu, kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu; Nitakusifu kwa kinubi, Ee MUNGU, Mungu wangu. 5 Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.

Zaburi 44

1 Ee Mungu, tumesikia kwa masikio yetu Baba zetu wametuambia, Matendo uliyoyatenda siku zao, siku za kale. 2 Wewe kwa mkono wako uliwafukuza mataifa, Ukawakalisha wao. Wewe uliwatesa watu wa nchi, Ukawaeneza wao. 3 Maana si kwa upanga wao walivyoimiliki nchi, Wala si mkono wao uliowaokoa; Bali mkono wako wa kuume, naam, mkono wako, Na nuru ya uso wako, kwa kuwa uliwaridhia. 4 Ee Mungu, Wewe ndiwe mfalme wangu, Uagize mambo ya wokovu kwa Yakobo. 5 Kwa nguvu zako tutawaangusha watesi wetu; Kwa jina lako tutawakanyaga watupingao. 6 Maana sitautumainia upinde wangu, Wala upanga wangu hautaniokoa. 7 Bali Wewe ndiwe uliyetuokoa na watesi wetu; Na watuchukiao umewaaibisha. 8 Tumejisifia Mungu mchana kutwa, Na jina lako tutalishukuru milele. 9 Lakini umetutupa, umetufedhehesha, Wala hutoki na majeshi yetu. 10 Waturudisha nyuma tukampa mtesi kisogo, Na watuchukiao wanajipatia mateka. 11 Umetutoa kama kondoo tuwe chakula, Na kututawanya kati ya mataifa. 12 Wawauza watu wako bila kupata mali, Wala hukupata faida kwa thamani yao. 13 Umetufanya kuwa lawama kwa jirani zetu, Mzaha na dhihaka kwao wanaotuzunguka. 14 Umetufanya kuwa mithali kwa mataifa, Sababu ya kutikisa kichwa kwa watu wa nchi. 15 Mchana kutwa fedheha yangu i mbele yangu, Na haya ya uso wangu imenifunika, 16 Kwa sauti ya mwenye kulaumu na kukufuru, Kwa sababu ya adui na mjilipiza kisasi. 17 Haya yote yametupata, bali hatukukusahau, Wala hatukulihalifu agano lako. 18 Hatukuiacha mioyo yetu irudi nyuma, Wala hatua zetu hazikuiacha njia yako. 19 Hata utuponde katika kao la mbwa-mwitu, Na kutufunika kwa uvuli wa mauti. 20 Ikiwa tumelisahau jina la Mungu wetu, Au kumnyoshea mungu mgeni mikono yetu; 21 Je! Mungu hatalichunguza neno hilo? Maana ndiye azijuaye siri za moyo. 22 Hasha! Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa; Tunafanywa kondoo waendao kuchinjwa. 23 Amka, Bwana, mbona umelala? Ondoka, usitutupe kabisa. 24 Mbona unatuficha uso wako, Na kusahau kuonewa na kudhulumiwa kwetu? 25 Maana nafsi yetu imeinama mavumbini, Tumbo letu limegandamana na nchi. 26 Uondoke, uwe msaada wetu, Utukomboe kwa ajili ya fadhili zako.

Zaburi 45

1 Moyo wangu umefurika kwa neno jema, Mimi nasema niliyomfanyizia mfalme; Ulimi wangu ni kalamu ya mwandishi mstadi. 2 Wewe u mzuri sana kuliko wanadamu; Neema imemiminiwa midomoni mwako, Kwa hiyo Mungu amekubariki hata milele. 3 Jifungie upanga wako pajani, wewe uliye hodari, Utukufu ni wako na fahari ni yako. 4 Katika fahari yako usitawi uendelee Kwa ajili ya kweli na upole na haki Na mkono wako wa kuume Utakufundisha mambo ya kutisha. 5 Mishale yako ni mikali, watu huanguka chini yako; Imo mioyoni mwa adui za mfalme. 6 Kiti chako cha enzi, Mungu, ni cha milele na milele, Fimbo ya ufalme wako ni fimbo ya adili. 7 Umeipenda haki; Umeichukia dhuluma. Kwa hiyo MUNGU, Mungu wako, amekupaka mafuta, Mafuta ya furaha kuliko wenzako. 8 Mavazi yako yote hunukia manemane Na udi na mdalasini. Katika majumba ya pembe Vinubi vimekufurahisha. 9 Binti za wafalme wamo Miongoni mwa akina bibi wako wastahiki. Mkono wako wa kuume amesimama malkia Amevaa dhahabu ya Ofiri. 10 Sikia, binti, utazame, utege sikio lako, Uwasahau watu wako na nyumba ya baba yako. 11 Naye mfalme atautamani uzuri wako, Maana ndiye bwana wako, nawe umsujudie. 12 Na binti Tiro analeta kipawa chake, Nao matajiri wa watu watajipendekeza kwako. 13 Binti mfalme yumo ndani ana fahari tupu, Mavazi yake ni ya nyuzi za dhahabu. 14 Atapelekwa kwa mfalme Na mavazi yaliyofumwa kwa uzuri. Wanawali wenzake wanaomfuata, Watapelekwa kwako. 15 Watapelekwa kwa furaha na shangwe, Na kuingia katika nyumba ya mfalme. 16 Badala ya baba zako watakuwapo watoto wako, Utawafanya kuwa wakuu katika nchi zote. 17 Jina lako nitalifanya kuwa kumbukumbu Katika vizazi vyote. Kwa hiyo mataifa watakushukuru Milele na milele.

Zaburi 46

1 Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. 2 Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. 3 Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. 4 Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. 5 Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema. 6 Mataifa yalighadhibika, falme zikataharuki; Alitoa sauti yake, nchi ikayeyuka. 7 Bwana wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu. 8 Njoni myatazame matendo ya Bwana, Jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. 9 Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; Avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari. 10 Acheni, mjue ya kuwa Mimi ni Mungu, Nitakuzwa katika mataifa, nitakuzwa katika nchi. 11 Bwana wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.

Zaburi 47

1 Enyi watu wote, pigeni makofi, Mpigieni Mungu kelele kwa Sauti ya shangwe. 2 Kwa kuwa Bwana Aliye juu, mwenye kuogofya, Ndiye mfalme mkuu juu ya dunia yote. 3 Atawatiisha watu wa nchi chini yetu, Na mataifa chini ya miguu yetu. 4 Atatuchagulia urithi wetu, Fahari ya Yakobo ambaye alimpenda. 5 Mungu amepaa kwa kelele za shangwe, Bwana kwa sauti ya baragumu. 6 Mwimbieni Mungu, naam, imbeni; Mwimbieni mfalme wetu, naam, imbeni. 7 Maana Mungu ndiye mfalme wa dunia yote, Imbeni kwa akili. 8 Mungu awamiliki mataifa, Mungu ameketi katika kiti chake kitakatifu. 9 Wakuu wa watu wamekusanyika, Wawe watu wa Mungu wa Ibrahimu. Maana ngao za dunia zina Mungu, Ametukuka sana.

Zaburi 48

1 Bwana ndiye aliye mkuu, Na mwenye kusifiwa sana. Katika mji wa Mungu wetu, Katika mlima wake mtakatifu. 2 Kuinuka kwake ni mzuri sana, Ni furaha ya dunia yote. Mlima Sayuni pande za kaskazini, Mji wa Mfalme mkuu. 3 Mungu katika majumba yake Amejijulisha kuwa ngome. 4 Maana, tazama, wafalme walikusanyika; Walipita wote pamoja. 5 Waliona, mara wakashangaa; Wakafadhaika na kukimbia. 6 Papo hapo tetemeko liliwashika, Utungu kama wa mwanamke azaaye. 7 Kwa upepo wa mashariki Wavunja jahazi za Tarshishi. 8 Kama tulivyosikia, ndivyo tulivyoona, Katika mji wa Bwana wa majeshi. Mji wa Mungu wetu; Mungu ataufanya imara hata milele. 9 Tumezitafakari fadhili zako, Ee Mungu, Katikati ya hekalu lako. 10 Kama lilivyo jina lako, Ee Mungu, Ndivyo na sifa yako hata miisho ya dunia. Mkono wako wa kuume umejaa haki; 11 Na ufurahi mlima Sayuni. Binti za Yuda na washangilie Kwa sababu ya hukumu zako. 12 Tembeeni katika Sayuni, Uzungukeni mji, Ihesabuni minara yake, 13 Tieni moyoni boma zake, Yafikirini majumba yake, Mpate kuwaambia kizazi kitakachokuja. 14 Kwa maana ndivyo alivyo MUNGU, Mungu wetu. Milele na milele Yeye ndiye atakayetuongoza.

Zaburi 49

1 Sikieni haya, enyi mataifa yote; Sikilizeni, ninyi nyote mnaokaa duniani. 2 Watu wakuu na watu wadogo wote pia, Tajiri na maskini wote pamoja. 3 Kinywa changu kitanena hekima, Na fikira za moyo wangu zitakuwa za busara. 4 Nitatega sikio langu nisikie mithali, Na kufumbua fumbo langu kwa kinubi 5 Kwa nini niogope siku za uovu, Ubaya ukinizunguka miguuni pangu? 6 Wa hao wanaozitumainia mali zao, Na kujisifia wingi wa utajiri wao; 7 Hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, Wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake, 8 (Maana fidia ya nafsi zao ina gharama, Wala hana budi kuiacha hata milele;) 9 ili aishi sikuzote asilione kaburi. 10 Naam, ataliona, hata wenye hekima hufa; Mpumbavu na mjinga hupotea pamoja, Na kuwaachia wengine mali zao. 11 Makaburi ni nyumba zao hata milele, Maskani zao vizazi hata vizazi. Hao waliotaja mashamba yao Kwa majina yao wenyewe. 12 Lakini mwanadamu hadumu katika heshima, Bali amefanana na wanyama wapoteao. 13 Hiyo ndiyo njia yao, ujinga wao, Nao walioko baada yao huyaridhia maneno yao. 14 Kama kondoo wamewekwa kwenda kuzimu, Na mauti itawachunga; Watu wanyofu watawamiliki asubuhi; Umbo lao litachakaa, kao lao ni kuzimu. 15 Bali Mungu atanikomboa nafsi yangu, Atanitoa mkononi mwa kuzimu, maana atanikaribisha. 16 Usiogope mtu atakapopata utajiri, Na fahari ya nyumba yake itakapozidi. 17 Maana atakapokufa hatachukua cho chote; Utukufu wake hautashuka ukimfuata. 18 Ajapojibariki nafsi yake alipokuwa hai, Na watu watakusifu ukijitendea mema, 19 Atakwenda kwenye kizazi cha baba zake Hawataona nuru hata milele. 20 Mwanadamu mwenye heshima, iwapo hana akili, Amefanana na wanyama wapoteao.

Zaburi 50

1 Mungu, Mungu Bwana, amenena, ameiita nchi, Toka maawio ya jua hata machweo yake. 2 Tokea Sayuni, ukamilifu wa uzuri, Mungu amemulika. 3 Mungu wetu atakuja wala hatanyamaza, Moto utakula mbele zake, na tufani yavuma sana ikimzunguka pande zote. 4 Ataziita mbingu zilizo juu, Na nchi pia awahukumu watu wake. 5 Nikusanyieni wacha Mungu wangu Waliofanya agano nami kwa dhabihu. 6 Na mbingu zitatangaza haki yake, Kwa maana Mungu ndiye aliye hakimu. 7 Sikieni, enyi watu wangu, nami nitanena, Mimi nitakushuhudia, Israeli; Mimi ndimi niliye MUNGU, Mungu wako. 8 Sitakukemea kwa ajili ya dhabihu zako, Na kafara zako ziko mbele zangu daima. 9 Sitatwaa ng'ombe katika nyumba yako, Wala beberu katika mazizi yako. 10 Maana kila hayawani ni wangu, Na makundi juu ya milima elfu. 11 Nawajua ndege wote wa milima, Na wanyama wote wa mashamba ni wangu 12 Kama ningekuwa na njaa singekuambia, Maana ulimwengu ni wangu, navyo viujazavyo. 13 Je! Nile nyama ya mafahali! Au ninywe damu ya mbuzi! 14 Mtolee Mungu dhabihu za kushukuru; Mtimizie Aliye juu nadhiri zako. 15 Ukaniite siku ya mateso; Nitakuokoa, na wewe utanitukuza. 16 Bali mtu asiye haki, Mungu amwambia, Una nini wewe kuitangaza sheria yangu, Na kuliweka agano langu kinywani mwako? 17 Maana wewe umechukia maonyo, Na kuyatupa maneno yangu nyuma yako. 18 Ulipomwona mwivi ulikuwa radhi naye, Ukashirikiana na wazinzi. 19 Umekiachia kinywa chako kinene mabaya, Na ulimi wako watunga hila. 20 Umekaa na kumsengenya ndugu yako, Na mwana wa mama yako umemsingizia. 21 Ndivyo ulivyofanya, nami nikanyamaza; Ukadhani ya kuwa Mimi ni kama wewe. Walakini nitakukemea; Nitayapanga hayo mbele ya macho yako. 22 Yafahamuni hayo, Ninyi mnaomsahau Mungu, Nisije nikawararueni, Asipatikane mwenye kuwaponya. 23 Atoaye dhabihu za kushukuru, Ndiye anayenitukuza. Naye autengenezaye mwenendo wake, Nitamwonyesha wokovu wa Mungu.

Zaburi 51

1 Ee Mungu, unirehemu, Sawasawa na fadhili zako. Kiasi cha wingi wa rehema zako, Uyafute makosa yangu. 2 Unioshe kabisa na uovu wangu, Unitakase dhambi zangu. 3 Maana nimejua mimi makosa yangu Na dhambi yangu i mbele yangu daima. 4 Nimekutenda dhambi Wewe peke yako, Na kufanya maovu mbele za macho yako. Wewe ujulikane kuwa una haki unenapo, Na kuwa safi utoapo hukumu. 5 Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatiani. 6 Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni; Nawe utanijulisha hekima kwa siri, 7 Unisafishe kwa hisopo nami nitakuwa safi, Unioshe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji 8 Unifanye kusikia furaha na shangwe, Mifupa uliyoiponda ifurahi. 9 Usitiri uso wako usitazame dhambi zangu; Uzifute hatia zangu zote. 10 Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu 11 Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. 12 Unirudishie furaha ya wokovu wako; Unitegemeze kwa roho ya wepesi. 13 Nitawafundisha wakosaji njia zako, Na wenye dhambi watarejea kwako. 14 Ee MUNGU, Mungu wa wokovu wangu, Uniponye na damu za watu, Na ulimi wangu utaiimba haki yako. 15 Ee Bwana, uifumbue midomo yangu, Na kinywa changu kitazinena sifa zako. 16 Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa, Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa. 17 Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau. 18 Uitendee mema Sayuni kwa radhi yako, Uzijenge kuta za Yerusalemu. 19 Ndipo utakapopendezwa na dhabihu za haki, Na sadaka za kuteketezwa, na kafara. Ndipo watakapotoa ng'ombe Juu ya madhabahu yako.

Zaburi 52

1 Kwa nini kujisifia uovu, Ewe jabari? Wema wa Mungu upo sikuzote. 2 Ulimi wako watunga madhara, Kama wembe mkali, Ewe mwenye hila 3 Umependa mabaya kuliko mema, Na uongo kuliko kusema kweli. 4 Umependa maneno yote ya kupoteza watu, Ewe ulimi wenye hila. 5 Lakini Mungu atakuharibu hata milele; Atakuondolea mbali; Atakunyakua hemani mwako; Atakung'oa katika nchi ya walio hai. 6 Nao wenye haki wataona; Wataingiwa na hofu na kumcheka; 7 Kumbe! Huyu ndiye mtu yule, Asiyemfanya Mungu kuwa nguvu zake. Aliutumainia wingi wa mali zake, Na kujifanya hodari kwa madhara yake. 8 Bali mimi ni kama mzeituni Umeao katika nyumba ya Mungu. Nazitumainia fadhili za Mungu milele na milele. 9 Nitakushukuru milele kwa maana umetenda; Nitalingojea jina lako kwa kuwa ni jema; Mbele ya wacha Mungu wako.

Zaburi 53

1 Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wametenda uovu wa ufisadi na kuchukiza, Hakuna atendaye mema. 2 Toka mbinguni MUNGU aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu. 3 Kila mtu amepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja. 4 Je! Wafanyao maovu hawajui? Walao watu wangu kama walavyo mkate, Hawakumwita MUNGU. 5 Hapo waliingiwa na hofu pasipokuwapo hofu, Maana Mungu ameitawanya mifupa yake aliyekuhusuru. Umewatia aibu, Kwa sababu MUNGU amewadharau. 6 Laiti wokovu wa Israeli utoke katika Sayuni! MUNGU awarudishapo wafungwa wa watu wake; Yakobo atashangilia, Israeli atafurahi.

Zaburi 54

1 Ee Mungu, kwa jina lako uniokoe, Na kwa uweza wako unifanyie hukumu. 2 Ee Mungu, uyasikie maombi yangu, Uyasikilize maneno ya kinywa changu. 3 Kwa maana wageni wamenishambulia; Watu watishao wananitafuta nafsi yangu; Hawakumweka Mungu mbele yao. 4 Tazama, Mungu ndiye anayenisaidia; Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu. 5 Atawarudishia adui zangu ubaya wao; Uwaangamize kwa uaminifu wako. 6 Kwa ukunjufu wa moyo nitakutolea dhabihu; Ee Bwana, nitalishukuru jina lako, maana ni jema. 7 Kwa kuwa limeniokoa na kila taabu; Na jicho langu limeridhika Kwa kuwatazama adui zangu.

Zaburi 55

1 Ee Mungu, uisikilize sala yangu, Wala usijifiche nikuombapo rehema. 2 Unisikilize na kunijibu, Nimetanga-tanga nikilalama na kuugua. 3 Kwa sababu ya sauti ya adui, Kwa sababu ya dhuluma yake yule mwovu. Kwa maana wananitupia uovu, Na kwa ghadhabu wananiudhi. 4 Moyo wangu unaumia ndani yangu, Na hofu za mauti zimeniangukia. 5 Hofu na tetemeko limenijia, Na hofu kubwa imenifunikiza. 6 Nikasema, Ningekuwa na mbawa kama njiwa, Ningerukia mbali na kustarehe. 7 Ningekwenda zangu mbali, Ningetua jangwani. 8 Ningefanya haraka kuzikimbia Dhoruba na tufani. 9 Ee Bwana, uwaangamize, uzichafue ndimi zao, Maana nimeona dhuluma na fitina katika mji. 10 Mchana na usiku huzunguka kutani mwake; Uovu na taabu zimo ndani yake; 11 Tamaa mbaya zimo ndani yake; Dhuluma na hila haziondoki mitaani mwake. 12 Kwa maana aliyetukana si adui; Kama ndivyo, ningevumilia. Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye; Kama ndivyo, ningejificha asinione. 13 Bali ni wewe, mtu mwenzangu, Rafiki yangu, niliyejuana nawe sana. 14 Tulipeana shauri tamu; na kutembea Nyumbani mwa Mungu pamoja na mkutano. 15 Mauti na iwapate kwa ghafula, Na washuke kuzimu wangali hai, Maana uovu u makaoni mwao na katikati yao. 16 Nami nitamwita Mungu, Na Bwana ataniokoa; 17 Jioni, asubuhi, na adhuhuri nitalalama na kuugua, Naye ataisikia sauti yangu. 18 Ameiokoa nafsi yangu iwe salama, asinikaribie mtu, Maana walioshindana nami walikuwa wengi. 19 Mungu atasikia na kuwajibu; Ndiye Yeye akaaye tangu milele. Mageuzi ya mambo hayawapati hao, Kwa hiyo hawamchi Mungu. 20 Amenyosha mkono awadhuru waliopatana naye, Amelihalifu agano lake. 21 Kinywa chake ni laini kuliko siagi, Bali moyo wake ni vita. Maneno yake ni mororo kuliko mafuta, Bali hayo ni panga wazi. 22 Umtwike Bwana mzigo wako naye atakutegemeza, Hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele. 23 Nawe, Ee Mungu, utawatelemsha, Walifikilie shimo la uharibifu; Watu wa damu na hila hawataishi nusu ya siku zao, Bali mimi nitakutumaini Wewe.

Zaburi 56

1 Mungu, unirehemu, maana yuko atakaye kunimeza, Mchana kutwa ananionea akileta vita. 2 Adui zangu wanataka kunimeza mchana kutwa, Maana waletao vita juu yangu kwa kiburi ni wengi. 3 Siku ya hofu yangu nitakutumaini Wewe; 4 Kwa msaada wa MUNGU nitalisifu neno lake. Nimemtumaini Mungu, sitaogopa; Mwenye mwili atanitenda nini? 5 Mchana kutwa wanapotosha maneno yangu, Mawazo yao yote ni juu yangu kunitakia mabaya. 6 Hukutanika, hujificha, huziangalia nyayo zangu, Kwa kuwa wameniotea nafsi yangu. 7 Je! Wataokoka kwa uovu wao? Ee Mungu, uwaangamize kwa hasira yako. 8 Umehesabu kutanga-tanga kwangu; Uyatie machozi yangu katika chupa yako; (Je! Hayamo katika kitabu chako?) 9 Ndipo adui zangu watarudi nyuma siku ile niitapo. Neno hili najua kuwa MUNGU yu upande wangu; 10 Kwa msaada wa MUNGU nitalisifu neno lake. Kwa msaada wa Bwana nitalisifu neno lake. 11 Nimemtumaini Mungu, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? 12 Ee Mungu, nadhiri zako zi juu yangu; Nitakutolea dhabihu za kushukuru. 13 Maana umeniponya nafsi yangu na mauti; Je! Hukuizuia miguu yangu isianguke? Ili nienende mbele za Mungu Katika nuru ya walio hai.

Zaburi 57

1 Unirehemu, Ee Mungu, unirehemu mimi, Maana nafsi yangu imekukimbilia Wewe. Nitaukimbilia uvuli wa mbawa zako, Hata misiba hii itakapopita. 2 Nitamwita MUNGU Aliye juu, Mungu anitimiziaye mambo yangu. 3 Atapeleka toka mbinguni na kuniokoa, Atukanapo yule atakaye kunimeza. Mungu atazipeleka Fadhili zake na kweli yake 4 Nafsi yangu i kati ya simba, Nitastarehe kati yao waliowaka moto. Wanadamu meno yao ni mikuki na mishale, Na ndimi zao ni upanga mkali. 5 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako. 6 Wameweka wavu ili kuninasa miguu; Nafsi yangu imeinama; Wamechimba shimo mbele yangu; Wametumbukia ndani yake! 7 Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Moyo wangu u thabiti. Nitaimba, nitaimba zaburi, 8 Amka, utukufu wangu. Amka, kinanda na kinubi, Nitaamka alfajiri. 9 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, Nitakuimbia zaburi kati ya mataifa. 10 Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni. 11 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako.

Zaburi 58

1 Ni kweli, enyi wakuu, mnanena haki? Enyi wanadamu, mnahukumu kwa adili? 2 Sivyo! Mioyoni mwenu mnatenda maovu; Katika nchi mnapima udhalimu wa mikono yenu. 3 Wasio haki wamejitenga tangu kuzaliwa kwao; Tangu tumboni wamepotea, wakisema uongo. 4 Sumu yao, mfano wake ni sumu ya nyoka; Mfano wao ni fira kiziwi azibaye sikio lake. 5 Asiyeisikiliza sauti ya waganga, Ijapo wanafanya uganga kwa ustadi. 6 Ee Mungu, uyavunje meno yao vinywani mwao; Ee Bwana, uyavunje magego ya wana-simba. 7 Na watoweke kama maji yapitayo kwa kasi; Akiielekeza mishale yake, iwe imetiwa ubutu. 8 Kama konokono ayeyukaye na kutoweka, Kama mimba iliyoharibika, isiyoliona jua, 9 Kabla ya masufuria yenu kupata moto wa miiba, Ataipeperusha kama chamchela, Iliyo mibichi na iliyo moto. 10 Mwenye haki atafurahi akionapo kisasi; Ataiosha miguu yake katika damu ya wasio haki. 11 Na mwanadamu atasema, Hakika iko thawabu yake mwenye haki. Hakika yuko Mungu Anayehukumu katika dunia.

Zaburi 59

1 Ee Mungu wangu, uniponye na adui zangu, Uniinue juu yao wanaoshindana nami. 2 Uniponye nao wafanyao maovu, Uniokoe na watu wa damu. 3 Kwa maana wanaiotea nafsi yangu; Wenye nguvu wamenikusanyikia; Ee Bwana, si kwa kosa langu, Wala si kwa hatia yangu. 4 Bila kosa langu huenda mbio, hujiweka tayari; Uamke uonane nami, na kutazama. 5 Na Wewe, Bwana, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, uamke. Uwapatilize mataifa yote; Usiwarehemu waovu wafanyao uovu hata mmoja. 6 Wakati wa jioni hurudi, hulia kama mbwa, Na kuzunguka-zunguka mjini. 7 Tazama, kwa vinywa vyao huteuka, Midomoni mwao mna panga, Kwa maana ni nani asikiaye? 8 Na Wewe, Bwana, utawacheka, Utawadhihaki mataifa yote. 9 Ee nguvu zangu, nitakungoja Wewe, Maana Mungu ndiye aliye ngome yangu 10 Mungu wa fadhili zangu atanitangulia, Mungu atanijalia kuwatazama adui zangu. 11 Usiwaue, watu wangu wasije wakasahau; Uwatawanye kwa uweza wako, Na kuwaangamiza, Ee Bwana, ngao yetu. 12 Kwa dhambi ya kinywa chao, Na kwa neno la midomo yao, Wanaswe kwa kiburi chao, Kwa ajili ya kulaani na uongo wasemao. 13 Uwakomeshe kwa hasira, Uwakomeshe watoweke, Wajue ya kuwa Mungu atawala katika Yakobo, Na hata miisho ya dunia. 14 Wakati wa jioni hurudi, hulia kama mbwa, Na kuzunguka-zunguka mjini. 15 Watatanga-tanga hao wakitafuta chakula; Wasiposhiba watakesha usiku kucha. 16 Nami nitaziimba nguvu zako asubuhi, Nitaziimba fadhili zako kwa furaha. Kwa kuwa ndiwe uliyekuwa ngome yangu, Na makimbilio siku ya shida yangu. 17 Ee nguvu zangu, nitakuimbia kwa furaha, Maana Mungu ndiye aliye ngome yangu, Mungu wa fadhili zangu.

Zaburi 60

1 Ee Mungu, umetutupa na kututawanya, Umekuwa na hasira, uturudishe tena. 2 Umeitetemesha nchi na kuipasua, Upaponye palipobomoka, maana inatikisika. 3 Umewaonyesha watu wako mazito, Na kutunywesha mvinyo ya kutuyumbisha. 4 Umewapa wakuogopao bendera, Ili itwekwe kwa ajili ya kweli. 5 Ili wapenzi wako waopolewe, Uokoe kwa mkono wako wa kuume, utuitikie. 6 Mungu amenena kwa utakatifu wake, Nami nitashangilia. Nitaigawanya Shekemu, Nitalipima bonde la Sukothi. 7 Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu, Na Efraimu ni nguvu ya kichwa changu. Yuda ni fimbo yangu ya kifalme, 8 Moabu ni bakuli langu la kunawia. Nitamtupia Edomu kiatu changu, Na kumpigia Filisti kelele za vita. 9 Ni nani atakayenipeleka hata mji wenye boma? Ni nani atakayeniongoza hata Edomu? 10 Ee Mungu, si Wewe uliyetutupa? Wala, Ee Mungu, hutoki na majeshi yetu? 11 Utuletee msaada juu ya mtesi, Maana wokovu wa binadamu haufai. 12 Kwa msaada wa Mungu tutatenda makuu, Maana Yeye atawakanyaga watesi wetu.

Zaburi 61

1 Ee Mungu, ukisikie kilio changu, Uyasikilize maombi yangu. 2 Toka mwisho wa nchi nitakulilia nikizimia moyo, Uniongoze juu ya mwamba nisioweza kuupanda. 3 Kwa maana ulikuwa kimbilio langu, Ngome yenye nguvu adui asinipate. 4 Nitakaa katika hema yako milele, Nitaikimbilia sitara ya mbawa zako 5 Maana Wewe, Mungu, umezisikia nadhiri zangu. Umewapa urithi wao waliogopao jina lako. 6 Utaziongeza siku za mfalme, Miaka yake itakuwa kama vizazi vingi. 7 Atakaa mbele za Mungu milele, Ziagize fadhili na kweli zimhifadhi. 8 Ndivyo nitakavyoliimbia jina lako daima, Ili niondoe nadhiri zangu kila siku.

Zaburi 62

1 Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake. 2 Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. 3 Hata lini mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama kitalu kilicho tayari kuanguka, 4 Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo chake; Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani. 5 Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake. 6 Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. 7 Kwa Mungu wokovu wangu, Na utukufu wangu; Mwamba wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa Mungu. 8 Enyi watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio letu. 9 Hakika binadamu ni ubatili, Na wenye cheo ni uongo, Katika mizani huinuka; Wote pamoja ni hafifu kuliko ubatili. 10 Msiitumainie dhuluma, Wala msijivune kwa unyang'anyi; Mali izidipo msiiangalie sana moyoni. 11 Mara moja amenena Mungu; Mara mbili nimeyasikia haya, Ya kuwa nguvu zina Mungu, 12 Na fadhili ziko kwako, Ee Bwana; Maana ndiwe umlipaye kila mtu Sawasawa na haki yake.

Zaburi 63

1 Ee MUNGU, Mungu wangu, nitakutafuta mapema, Nafsi yangu inakuonea kiu, Mwili wangu wakuonea shauku, Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji. 2 Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu, Nizione nguvu zako na utukufu wako. 3 Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai; Midomo yangu itakusifu. 4 Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai; Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu. 5 Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono; Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. 6 Ninapokukumbuka kitandani mwangu, Nakutafakari Wewe makesha yote ya usiku. 7 Maana Wewe umekuwa msaada wangu, Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia. 8 Nafsi yangu inakuandama sana; Mkono wako wa kuume unanitegemeza. 9 Bali waitafutao nafsi yangu, ili kuiharibu, Wataingia pande za nchi zilizo chini. 10 Watatolewa wafe kwa nguvu za upanga, Watakuwa riziki za mbwa-mwitu. 11 Bali mfalme atamfurahia Mungu, Kila aapaye kwa Yeye atashangilia, Kwa maana vinywa vya waongo vitafumbwa.

Zaburi 64

1 Mungu, uisikie sauti yangu katika malalamiko yangu; Unilinde uhai wangu na hofu ya adui. 2 Utanificha mbali na shauri la siri la watenda mabaya, Mbali na ghasia ya watu wafanyao maovu; 3 Waliounoa ulimi wao kama upanga, Wameielekeza mishale yao, maneno ya uchungu, 4 Wapate kumpiga mkamilifu faraghani, Kwa ghafula humpiga wala hawaogopi. 5 Walijifanya hodari katika jambo baya; Hushauriana juu ya kutega mitego; Husema, Ni nani atakayeiona? 6 Hutunga maovu; husema, Tumefanya shauri kamili; Na mawazo ya ndani ya kila mmoja wao, Na moyo wake, huwa siri kabisa. 7 Kwa hiyo Mungu atawapiga shabaha, Kwa mshale mara watapigwa. 8 Ndivyo watakavyokwazwa, Ulimi wao wenyewe ukishindana nao. Wote wawaonao watatikisa kichwa. 9 Na watu wote wataogopa, Wataitangaza kazi ya Mungu, Na kuyafahamu matendo yake. 10 Mwenye haki atamfurahia Bwana na kumkimbilia, Na wote wenye moyo wa adili watajisifu.

Zaburi 65

1 Ee Mungu, sifa zakulaiki katika Sayuni, Na kwako Wewe itaondolewa nadhiri. 2 Wewe usikiaye kuomba, Wote wenye mwili watakujia. 3 Ingawa maovu mengi yanamshinda, Wewe utayafunika maasi yetu. 4 Heri mtu yule umchaguaye, Na kumkaribisha akae nyuani mwako. Na tushibe wema wa nyumba yako, Patakatifu pa hekalu lako. 5 Kwa mambo ya kutisha utatujibu, Katika haki, Ee Mungu wa wokovu wetu. Wewe uliye tumaini la miisho yote ya dunia, Na la bahari iliyo mbali sana, 6 Milima waiweka imara kwa nguvu zako, Huku ukijifunga uweza kama mshipi. 7 Wautuliza uvumi wa bahari, Uvumi wa mawimbi yake, Na ghasia ya mataifa; 8 Kwa hiyo wakaao mbali kabisa huogopa ishara zako; Milango ya asubuhi na jioni waifurahisha. 9 Umeijilia nchi na kuisitawisha, Umeitajirisha sana; Mto wa Mungu umejaa maji; Wawaruzuku watu nafaka Maana ndiwe uitengenezaye ardhi. 10 Matuta yake wayajaza maji; Wapasawazisha palipoinuka, Wailainisha nchi kwa manyunyu; Waibariki mimea yake. 11 Umeuvika mwaka taji ya wema wako; Mapito yako yadondoza unono. 12 Huyadondokea malisho ya nyikani, Na vilima vyajifunga furaha. 13 Na malisho yamevikwa kondoo, Na mabonde yamepambwa nafaka, Yanashangilia, naam, yanaimba.

Zaburi 66

1 Mpigie Mungu kelele za shangwe, nchi yote, 2 Imbeni utukufu wa jina lake, Tukuzeni sifa zake. 3 Mwambieni Mungu, Matendo yako yatisha kama nini! Kwa ajili ya wingi wa nguvu zako, Adui zako watakuja kunyenyekea mbele zako. 4 Nchi yote itakusujudia na kukuimbia, Naam, italiimbia jina lako. 5 Njoni yatazameni matendo ya Mungu; Hutisha kwa mambo awatendayo wanadamu; 6 Aligeuza bahari ikawa nchi kavu; Katika mto walivuka kwa miguu; Huko ndiko mlikomfurahia. 7 Atawala kwa uweza wake milele; Macho yake yanaangalia mataifa; Waasio wasijitukuze nafsi zao. 8 Enyi mataifa, mtukuzeni Mungu wetu, Itangazeni sauti ya sifa zake; 9 Aliyeiweka nafsi yetu katika uhai, Wala hakuuacha mguu wetu usogezwe. 10 Kwa maana umetupima, Ee Mungu, Umetujaribu inavyojaribiwa fedha. 11 Ulituingiza ndani ya wavu, Na kuweka viunoni mwetu mzigo uliotulemea. 12 Uliwapandisha watu Juu ya vichwa vyetu. Tulipita motoni na majini; Ukatutoa na kutuleta kunako wingi. 13 Nitaingia nyumbani mwako na kafara; Nitaondoa kwako nadhiri zangu; 14 Ambazo midomo yangu ilizinena; Kinywa changu kikazisema nilipokuwa taabuni. 15 Kafara za vinono nitakutolea, Pamoja na fukizo la kondoo waume, Nitatoa ng'ombe pamoja na mbuzi. 16 Njoni, sikieni, ninyi nyote mnaomcha Mungu, Nami nitayatangaza aliyonitendea roho yangu. 17 Nalimwita kwa kinywa changu, Na sifa kuu zilikuwa chini ya ulimi wangu. 18 Kama ningaliwaza maovu moyoni mwangu, Bwana asingesikia. 19 Hakika Mungu amesikia; Ameisikiliza sauti ya maombi yangu. 20 Na ahimidiwe Mungu asiyeyakataa maombi yangu, Wala kuniondolea fadhili zake.

Zaburi 67

1 Mungu na atufadhili na kutubariki, Na kutuangazia uso wake. 2 Njia yake ijulike duniani, Wokovu wake katikati ya mataifa yote. 3 Watu na wakushukuru, Ee Mungu, Watu wote na wakushukuru. 4 Mataifa na washangilie, Naam, waimbe kwa furaha, Maana kwa haki utawahukumu watu, Na kuwaongoza mataifa walioko duniani. 5 Watu na wakushukuru, Ee Mungu, Watu wote na wakushukuru. 6 Nchi imetoa mazao yake MUNGU, Mungu wetu, ametubariki. 7 Mungu atatubariki sisi; Miisho yote ya dunia itamcha Yeye.

Zaburi 68

1 Mungu huondoka, adui zake wakatawanyika, Nao wamchukiao huukimbia uso wake. 2 Kama moshi upeperushwavyo, Ndivyo uwapeperushavyo wao; Kama nta iyeyukavyo mbele ya moto, Ndivyo waovu wapoteavyo usoni pa Mungu. 3 Bali wenye haki hufurahi, Na kuushangilia uso wa Mungu, Naam, hupiga kelele kwa furaha. 4 Mwimbieni Mungu, lisifuni jina lake, Mtengenezeeni njia ya barabara, Apitaye majangwani kama mpanda farasi; Jina lake ni YAHU; shangilieni mbele zake. 5 Baba wa yatima na mwamuzi wa wajane, Mungu katika kao lake takatifu. 6 Mungu huwakalisha wapweke nyumbani; Huwatoa wafungwa wakae hali ya kufanikiwa; Bali wakaidi hukaa katika nchi kavu. 7 Ee Mungu, ulipotoka mbele ya watu wako, Ulipopita nyikani, 8 Nchi ilitetemeka Naam, mbingu zilidondoka usoni pa Mungu; Hata Sinai usoni pa Mungu; Mungu wa Israeli. 9 Ee Mungu, ulinyesha mvua ya neema; Urithi wako ulipochoka uliutia nguvu. 10 Kabila yako ilifanya kao lake huko; Ee Mungu, kwa wema wako uliwaruzuku walioonewa. 11 Bwana analitoa neno lake; Wanawake watangazao habari ni jeshi kubwa; 12 Wafalme wa majeshi wanakimbia, wanakimbia; Na mwanamke akaaye nyumbani agawa nyara. 13 Kwa nini kulala mazizini arukapo hua, Mbawa zake ziking'aa kama fedha Na manyoya yake kama dhahabu? 14 Mwenyezi Mungu alipotawanya wafalme huko, Kulinyesha theluji katika Salmoni. 15 Ni mlima wa Mungu mlima Bashani, Ni mlima mrefu mlima Bashani. 16 Enyi milima mirefu, kwani kuutazama kwa wivu Mlima alioutamani Mungu akae juu yake? Naam, Bwana atakaa juu yake milele. 17 Magari ya Mungu ni ishirini elfu, maelfu maelfu; Bwana yumo kati yao kama katika Sinai, Katika patakatifu. 18 Wewe umepaa juu, umeteka mateka, Umepewa vipawa katikati ya wanadamu; Naam, hata na wakaidi, Bwana Mungu akae nao. 19 Na ahimidiwe Bwana, Siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu; Mungu ndiye wokovu wetu. 20 Mungu kwetu sisi ni Mungu wa kuokoa; Na njia za kutoka mautini zina YEHOVA Bwana. 21 Naam, Mungu atakipasua kichwa cha adui zake, Utosi wenye nywele wa mtu afulizaye kukosa. 22 Bwana alisema, Kutoka Bashani nitawarudisha, Nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari; 23 Uuchovye mguu wako katika damu ya adui zako, Na ulimi wa mbwa zako upate sehemu yake. 24 Ee Mungu, wameiona miendo yako; Miendo ya Mungu wangu, Mfalme wangu, katika patakatifu 25 Waimbaji hutangulia, nyuma yao wapigao vinanda, Kati ya wanawali wapiga matari. 26 Mhimidini Mungu katika mikutano, Bwana katika makusanyiko ya Israeli. 27 Yuko Benyamini mdogo, mtawala wao; Wakuu wa Yuda, kundi lao; Wakuu wa Zabuloni; Wakuu wa Naftali. 28 Ee Mungu, uziamuru nguvu zako; Ee Mungu, uwe hodari uliyetufanyia makuu. 29 Kwa ajili ya hekalu lako Yerusalemu Wafalme watakuletea hedaya. 30 Mkemee mnyama wa manyasini; Kundi la mafahali, na ndama za watu; Hata wanyenyekee na kuleta vipande vya fedha, Uwatawanye watu wapendao vita. 31 Masheki watakuja kutoka Misri, Kushi itamnyoshea Mungu mikono yake mara. 32 Enyi falme za dunia, mwimbieni Mungu, Msifuni Bwana kwa nyimbo. 33 Apandaye mbingu za mbingu za tangu milele; Aitoa sauti yake, sauti ya nguvu. 34 Mhesabieni Mungu nguvu; Enzi yake i juu ya Israeli; Na nguvu zake zi mawinguni. 35 Mungu ni mwenye kutisha Kutoka patakatifu pako. Ndiye Mungu wa Israeli; Yeye huwapa watu wake nguvu na uwezo. Na ahimidiwe Mungu.

Zaburi 69

1 Ee Mungu, uniokoe, Maana maji yamefika mpaka nafsini mwangu. 2 Ninazama katika matope mengi, Pasipowezekana kusimama. Nimefika penye maji ya vilindi, Mkondo wa maji unanigharikisha. 3 Nimechoka kwa kulia kwangu, Koo yangu imekauka. Macho yangu yamedhoofu Kwa kumngoja Mungu wangu. 4 Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua. 5 Ee Mungu, unajua upumbavu wangu, Wala hukufichwa dhambi yangu. 6 Wanaokungoja Wewe wasiaibishwe, Kwa ajili yangu, Bwana, MUNGU wa majeshi. Wanaokutafuta Wewe wasifedheheshwe, Kwa ajili yangu, Ee Mungu wa Israeli. 7 Maana kwa ajili yako nimestahimili laumu, Fedheha imenifunika uso wangu. 8 Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, Na msikwao kwa wana wa mama yangu. 9 Maana wivu wa nyumba yako umenila, Na laumu zao wanaokulaumu zimenipata. 10 Nilipolia na kuiadhibu roho yangu kwa kufunga, Ikawa laumu juu yangu. 11 Nilipofanya gunia kuwa nguo zangu, Nikawa mithali kwao. 12 Waketio langoni hunisema, Na nyimbo za walevi hunidhihaki. 13 Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana, Wakati ukupendezao; Ee Mungu, Kwa wingi wa fadhili zako unijibu, Katika kweli ya wokovu wako. 14 Uniponye kwa kunitoa matopeni, Wala usiniache nikazama. Na niponywe nao wanaonichukia, Na katika vilindi vya maji. 15 Mkondo usinigharikishe, wala vilindi visinimeze, Wala shimo lisifumbe kinywa chake juu yangu. 16 Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema, Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. 17 Wala usinifiche uso wako, mimi mtumishi wako, Maana mimi nimo taabuni, unijibu upesi. 18 Uikaribie nafsi yangu, uikomboe, Kwa sababu ya adui zangu unifidie. 19 Wewe umejua kulaumiwa kwangu, Na kuaibika na kufedheheka kwangu, Mbele zako Wewe wako watesi wangu wote. 20 Laumu imenivunja moyo, Nami ninaugua sana. Nikangoja aje wa kunihurumia, wala hakuna; Na wa kunifariji, wala sikumwona mtu. 21 Wakanipa uchungu kuwa chakula changu; Nami nilipokuwa na kiu wakaninywesha siki. 22 Meza yao mbele yao na iwe mtego; Naam, wakiwa salama na iwe tanzi. 23 Macho yao yatiwe giza wasione, Na viuno vyao uvitetemeshe daima. 24 Uimwage ghadhabu yako juu yao, Na ukali wa hasira yako uwapate. 25 Matuo yao na yawe ukiwa, Pasiwe na mtu wa kukaa hemani mwao. 26 Maana wanamwudhi mtu uliyempiga Wewe, Wanasimulia maumivu ya hao uliowatia jeraha. 27 Uwaongezee uovu juu ya uovu, Wala wasiingie katika haki yako. 28 Na wafutwe katika chuo cha uhai, Wala pamoja na wenye haki wasiandikwe. 29 Nami niliye maskini na mtu wa huzuni, Mungu, wokovu wako utaniinua. 30 Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo, Nami nitamtukuza kwa shukrani. 31 Nayo yatampendeza Bwana kuliko ng'ombe, Au ndama mwenye pembe na kwato. 32 Walioonewa watakapoona watafurahi; Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yenu ihuishwe. 33 Kwa kuwa Bwana huwasikia wahitaji, Wala hawadharau wafungwa wake. 34 Mbingu na nchi zimsifu, Bahari na vyote viendavyo ndani yake. 35 Maana Mungu ataiokoa Sayuni, na kuijenga miji ya Yuda, Na watu watakaa ndani yake na kuimiliki. 36 Wazao wa watumishi wake watairithi, Nao walipendao jina lake watakaa humo.

Zaburi 70

1 Ee Mungu, uniokoe, Ee Bwana, unisaidie hima. 2 Waaibike, wafedheheke, Wanaoitafuta nafsi yangu. Warudishwe nyuma, watahayarishwe, Wapendezwao na shari yangu. 3 Warudi nyuma, na iwe aibu yao, Wanaosema, Ewe! Ewe! 4 Washangilie, wakufurahie, Wote wakutafutao. Waupendao wokovu wako Waseme daima, Atukuzwe Mungu. 5 Nami ni maskini na mhitaji, Ee Mungu, unijilie kwa haraka. Ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu, Ee Bwana, usikawie.

Zaburi 71

1 Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele. 2 Kwa haki yako uniponye, uniopoe, Unitegee sikio lako, uniokoe. 3 Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu, Nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru niokolewe, Ndiwe genge langu na ngome yangu. 4 Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi, Katika mkono wake mwovu, mdhalimu, 5 Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, Tumaini langu tokea ujana wangu. 6 Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa, Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu, Ninakusifu Wewe daima. 7 Nimekuwa kitu cha ajabu kwa watu wengi, Na Wewe ndiwe kimbilio langu la nguvu. 8 Kinywa changu kitajazwa sifa zako, Na heshima yako mchana kutwa. 9 Usinitupe wakati wa uzee, Nguvu zangu zipungukapo usiniache. 10 Kwa maana adui zangu wananiamba, Nao wanaoniotea roho yangu hushauriana. 11 Wakisema, Mungu amemwacha, Mfuatieni, mkamateni, hakuna wa kumponya. 12 Ee Mungu, usiwe mbali nami; Ee Mungu wangu, fanya haraka kunisaidia. 13 Waaibishwe, watoweshwe, adui za nafsi yangu. Wavikwe laumu na aibu wanaonitakia mabaya. 14 Nami nitatumaini daima, Nitazidi kuongeza sifa zake zote. 15 Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake. 16 Nitakuja na mambo ya ajabu ya Bwana MUNGU; Nitawakumbusha watu haki yako Wewe peke yako. 17 Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu; Nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo. 18 Na hata nikiwa ni mzee mwenye mvi, Ee Mungu, usiniache. Hata niwaeleze watu wa kizazi hiki nguvu zako, Na kila atakayekuja uweza wako. 19 Na haki yako, Ee Mungu, Imefika juu sana. Wewe uliyefanya mambo makuu; Ee Mungu, ni nani aliye kama Wewe? 20 Wewe, uliyetuonyesha mateso mengi, mabaya, Utatuhuisha tena. Utatupandisha juu tena Tokea pande za chini ya nchi. 21 Laiti ungeniongezea ukuu! Urejee tena na kunifariji moyo. 22 Nami nitakushukuru kwa kinanda, Na kweli yako, Ee Mungu wangu. Nitakuimbia Wewe kwa kinubi, Ee Mtakatifu wa Israeli. 23 Midomo yangu itafurahi sana nikuimbiapo, Na nafsi yangu uliyoikomboa. 24 Ulimi wangu nao utasimulia Haki yako mchana kutwa. Kwa maana wameaibishwa, Wametahayarika, wanaonitakia mabaya.

Zaburi 72

1 Ee Mungu, mpe mfalme hukumu zako, Na mwana wa mfalme haki yako. 2 Atawaamua watu wako kwa haki, Na watu wako walioonewa kwa hukumu. 3 Milima itawazalia watu amani, Na vilima navyo kwa haki. 4 Atawahukumu walioonewa wa watu, Atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea. 5 Watakuogopa wakati wote wa kudumu jua, Na wakati wa kung'aa mwezi kizazi hata kizazi. 6 Atashuka kama mvua juu ya majani yaliyokatwa, Kama manyunyu yainyweshayo nchi. 7 Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, Na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. 8 Na awe na enzi toka bahari hata bahari, Toka Mto hata miisho ya dunia. 9 Wakaao jangwani na wainame mbele zake; Adui zake na warambe mavumbi. 10 Wafalme wa Tarshishi na visiwa na walete kodi; Wafalme wa Sheba na Seba na watoe vipawa. 11 Naam, wafalme wote na wamsujudie; Na mataifa yote wamtumikie. 12 Kwa maana atamkomboa mhitaji aliapo, Na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. 13 Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, Na nafsi za wahitaji ataziokoa. 14 Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, Na damu yao ina thamani machoni pake. 15 Basi na aishi; Na wampe dhahabu ya Sheba; Na wamwombee daima; Na kumbariki mchana kutwa. 16 Na uwepo wingi wa nafaka Katika ardhi juu ya milima; Matunda yake na yawaye-waye kama Lebanoni, Na watu wa mjini wasitawi kama majani ya nchi. 17 Jina lake na lidumu milele, Pindi ling'aapo jua jina lake liwe na wazao; Mataifa yote na wajibariki katika yeye, Na kumwita heri. 18 Na ahimidiwe Bwana, Mungu, Mungu wa Israeli, Atendaye miujiza Yeye peke yake; 19 Jina lake tukufu na lihimidiwe milele; Dunia yote na ijae utukufu wake. Amina na Amina. 20 Maombi ya Daudi mwana wa Yese yamekwisha.

Zaburi 73

1 Hakika Mungu ni mwema kwa Israeli, Kwa hao walio safi mioyo yao. 2 Nami miguu yangu ilikuwa karibu na kupotoka, Hatua zangu zilikuwa karibu na kuteleza. 3 Maana naliwaonea wivu wenye kujivuna, Nilipoiona hali ya amani ya wasio haki. 4 Maana hawana maumivu katika kufa kwao, Na mwili wao una nguvu. 5 Katika taabu ya watu hawamo, Wala hawapati mapigo pamoja na wanadamu. 6 Hivyo kiburi kimekuwa mkufu shingoni mwao, Jeuri huwavika kama nguo. 7 Macho yao hutokeza kwa kunenepa, Wameipita kadiri ya mawazo ya mioyo yao. 8 Hudhihaki, husimulia mabaya, Husimulia udhalimu kana kwamba wako juu. 9 Wameweka kinywa chao mbinguni, Na ulimi wao hutanga-tanga duniani. 10 Kwa hiyo watu wake hugeuka huko, Na maji yaliyojaa humezwa nao. 11 Nao husema, Mungu ajuaje? Yako maarifa kwake aliye juu? 12 Fahamu, ndivyo walivyo wasio haki, Na kwa kustarehe sikuzote wamepata mali nyingi. 13 Hakika nimejisafisha moyo wangu bure, Nimenawa mikono yangu kwa kutokukosa. 14 Maana mchana kutwa nimepigwa, Na kuadhibiwa kila asubuhi. 15 Kama ningalisema, Nitasimulia kama hayo; Kumbe! Ningaliwadanganya kizazi cha wana wako. 16 Nami nalifikiri jinsi ya kufahamu hayo; Ikawa taabu machoni pangu; 17 Hata nilipoingia katika patakatifu pa Mungu, Nikautafakari mwisho wao. 18 Hakika Wewe huwaweka penye utelezi, Huwaangusha mpaka palipoharibika. 19 Namna gani wamekuwa ukiwa mara! Wametokomea na kutoweshwa kwa utisho. 20 Ee Bwana, kama ndoto wakati wa kuamka, Uondokapo utaidharau sanamu yao. 21 Moyo wangu ulipoona uchungu, Viuno vyangu viliponichoma, 22 Nalikuwa kama mjinga, sijui neno; Nalikuwa kama mnyama tu mbele zako. 23 Walakini mimi ni pamoja nawe daima, Umenishika mkono wa kuume. 24 Utaniongoza kwa shauri lako, Na baadaye utanikaribisha kwa utukufu. 25 Ni nani niliye naye mbinguni, Wala duniani sina cha kupendeza ila Wewe. 26 Mwili wangu na moyo wangu hupunguka, Bali Mungu ni mwamba wa moyo wangu Na sehemu yangu milele. 27 Maana wajitengao nawe watapotea; Umewaangamiza wote waliokuacha Wewe. 28 Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; Nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU, Niyahubiri matendo yako yote.

Zaburi 74

1 Ee Mungu, mbona umetutupa milele? Kwa nini hasira yako inatoka moshi Juu ya kondoo wa malisho yako? 2 Ulikumbuke kusanyiko lako, Ulilolinunua zamani. Ulilolikomboa liwe kabila ya urithi wako, Mlima Sayuni ulioufanya maskani yako. 3 Upainulie miguu yako palipoharibika milele; Adui ameufanya kila ubaya katika patakatifu. 4 Watesi wako wamenguruma kati ya kusanyiko lako; Wameweka bendera zao ziwe alama. 5 Wanaonekana kama watu wainuao mashoka, Waikate miti ya msituni. 6 Na sasa nakishi yake yote pia Wanaivunja-vunja kwa mashoka na nyundo. 7 Wamepatia moto patakatifu pako; Wamelinajisi kao la jina lako hata chini. 8 Walisema mioyoni mwao, Na tuwaangamize kabisa; Mahali penye mikutano ya Mungu Wamepachoma moto katika nchi pia. 9 Hatuzioni ishara zetu, wala sasa hakuna nabii, Wala kwetu hakuna ajuaye, hata lini? 10 Ee Mungu, mtesi atalaumu hata lini? Adui alidharau jina lako hata milele? 11 Mbona unaurudisha mkono wako, Naam, mkono wako wa kuume, Uutoe kifuani mwako, Ukawaangamize kabisa. 12 Lakini Mungu ni mfalme wangu tokea zamani, Afanyaye mambo ya wokovu katikati ya nchi. 13 Wewe umeipasua bahari kwa nguvu zako, Umevivunja vichwa vya nyangumi juu ya maji. 14 Wewe uliviseta vichwa vya lewiathani, Awe chakula cha watu wa jangwani. 15 Wewe ulitokeza chemchemi na kijito; Wewe ulikausha mito yenye maji sikuzote. 16 Mchana ni wako, usiku nao ni wako, Ndiwe uliyeufanya mwanga na jua. 17 Wewe uliiweka mipaka yote ya dunia, Kaskazi na kusi Wewe ulizitengeneza. 18 Ee Bwana, uyakumbuke hayo, adui amelaumu, Na watu wapumbavu wamelidharau jina lako. 19 Usimpe mnyama mkali nafsi ya hua wako; Usiusahau milele uhai wa watu wako walioonewa. 20 Ulitafakari agano; Maana mahali penye giza katika nchi Pamejaa makao ya ukatili. 21 Aliyeonewa asirejee ametiwa haya, Mnyonge na mhitaji na walisifu jina lako. 22 Ee Mungu, usimame, ujitetee mwenyewe, Ukumbuke unavyotukanwa na mpumbavu mchana kutwa. 23 Usiisahau sauti ya watesi wako, Ghasia yao wanaokuondokea inapaa daima.

Zaburi 75

1 Ee Mungu, twakushukuru. Twakushukuru kwa kuwa Jina lako li karibu; Watu huyasimulia matendo yako ya ajabu. 2 Nitakapoufikia wakati ulioamriwa, Mimi nitahukumu hukumu za haki. 3 Ingawa dunia na wote wakaao humo wataharuki, Mimi mwenyewe nimezisimamisha nguzo zake. 4 Naliwaambia waliojivuna, Msijivune; Na wasio haki, Msiiinue pembe. 5 Msiiinue pembe yenu juu, Wala msinene kwa shingo ya kiburi. 6 Maana siko mashariki wala magharibi, Wala nyikani itokako heshima. 7 Bali Mungu ndiye ahukumuye; Humdhili huyu na kumwinua huyu. 8 Maana mkononi mwa Bwana mna kikombe, Na mvinyo yake inatoka povu; Kumejaa machanganyiko; Naye huyamimina. Na sira zake wasio haki wa dunia Watazifyonza na kuzinywa. 9 Bali mimi nitatangaza matendo yako milele, Nitamwimbia Mungu wa Yakobo. 10 Pembe zote za wasio haki nitazikata, Na pembe za mwenye haki zitainuka.

Zaburi 76

1 Katika Yuda Mungu amejulikana, Katika Israeli jina lake ni kuu. 2 Kibanda chake pia kiko Salemu, Na maskani yake iko Sayuni. 3 Huko ndiko alikoivunja mishale ya uta, Ngao, na upanga, na zana za vita. 4 Wewe U mwenye fahari na adhama, Toka milima ya mateka. 5 Wametekwa wenye moyo thabiti; Wamelala usingizi; Wala hawakuiona mikono yao Watu wote walio hodari. 6 Kwa kukemea kwako, Ee Mungu wa Yakobo, Gari na farasi wameshikwa na usingizi mzito. 7 Wewe ndiwe utishaye, naam, Wewe; Naye ni nani awezaye kusimama ufanyapo hasira? 8 Toka mbinguni ulitangaza hukumu; Nchi iliogopa, ikakaa kimya. 9 Mungu aliposimama ili kuhukumu Na kuwaokoa wapole wa dunia wote pia. 10 Maana hasira ya binadamu itakusifu, Masalio ya hasira utajifunga kama mshipi. 11 Wekeni nadhiri, mkaziondoe Kwa Bwana, Mungu wenu. Wote wanaomzunguka wamletee hedaya, Yeye astahiliye kuogopwa. 12 Yeye huzikata roho za wakuu; Na kuwatisha wafalme wa dunia.

Zaburi 77

1 Nimpazie Mungu sauti yangu, Naam, nimpazie Mungu, naye atanisikia. 2 Siku ya taabu yangu nalimtafuta Bwana; Mkono wangu ulinyoshwa usiku, haukulegea; Nafsi yangu ilikataa kufarijika. 3 Nilipotaka kumkumbuka Mungu nalifadhaika; Nilipotaka kutafakari roho yangu ilizimia. 4 Ulizishika kope za macho yangu zisifumbike; Naliona mashaka nisiweze kunena. 5 Nalifikiri habari za siku za kale, Miaka ya zamani zilizopita. 6 Nakumbuka wimbo wangu usiku, Nawaza moyoni mwangu, Roho yangu ikatafuta. 7 Je! Bwana atatupa milele na milele? Hatatenda fadhili tena kabisa? 8 Rehema zake zimekoma hata milele? Ahadi yake imekwisha hata vizazi vyote? 9 Mungu amesahau fadhili zake? Amezuia kwa hasira rehema zake? 10 Nikasema, Ndio udhaifu wangu huo; Lakini nitaikumbuka miaka ya mkono wa kuume wake Aliye juu. 11 Nitayakumbuka matendo ya Bwana; Naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. 12 Pia nitaitafakari kazi yako yote; Nitaziwaza habari za matendo yako. 13 Ee Mungu, njia yako i katika utakatifu; Ni nani aliye mungu mkuu kama Mungu? 14 Wewe ndiwe Mungu ufanyaye maajabu; Uliudhihirisha uweza wako kati ya mataifa. 15 Kwa mkono wako umewakomboa watu wako, Wana wa Yakobo na Yusufu. 16 Ee Mungu, yale maji yalikuona, Yale maji yalikuona, yakaogopa. Vilindi vya maji navyo vikatetemeka, 17 Mawingu yakamwaga maji. Mbingu nazo zikatoa sauti, Mishale yako nayo ikatapakaa. 18 Sauti ya radi yako ikawa katika kisulisuli; Umeme uliuangaza ulimwengu. Nchi ilitetemeka na kutikisika; 19 Njia yako ilikuwa katika bahari. Na mapito yako yalikuwa katika maji makuu; Hatua zako hazikujulikana. 20 Uliwaongoza watu wako kama kundi, Kwa mkono wa Musa na Haruni.

Zaburi 78

1 Enyi watu wangu, sikilizeni sheria yangu, Tegeni masikio kwa maneno ya kinywa changu. 2 Na nifunue kinywa changu kwa mithali, Niyatamke mafumbo ya kale. 3 Mambo tuliyoyasikia na kuyafahamu, Ambayo baba zetu walituambia. 4 Hayo hatutawaficha wana wao, Huku tukiwaambia kizazi kingine, Sifa za Bwana, na nguvu zake, Na mambo yake ya ajabu aliyoyafanya. 5 Maana alikaza ushuhuda katika Yakobo, Na sheria aliiweka katika Israeli. Aliyowaamuru baba zetu Wawajulishe wana wao, 6 Ili kizazi kingine wawe na habari, Ndio hao wana watakaozaliwa. Wasimame na kuwaambia wana wao 7 Wamwekee Mungu tumaini lao. Wala wasiyasahau matendo ya Mungu, Bali wazishike amri zake. 8 Naam, wasiwe kama baba zao, Kizazi cha ukaidi na uasi. Kizazi kisichojitengeneza moyo, Wala roho yake haikuwa amini kwa Mungu. 9 Wale Waefraimu, wenye silaha, wapiga upinde, Walirudi nyuma siku ya vita. 10 Hawakulishika agano la Mungu; Wakakataa kuenenda katika sheria yake; 11 Wakayasahau matendo yake, Na mambo yake ya ajabu aliyowaonyesha. 12 Mbele ya baba zao alifanya mambo ya ajabu, Katika nchi ya Misri, konde la Soani. 13 Aliipasua bahari akawavusha; Aliyasimamisha maji mfano wa chungu. 14 Akawaongoza kwa wingu mchana, Na usiku kucha kwa nuru ya moto. 15 Akapasua miamba jangwani; Akawanywesha maji mengi kama maji ya vilindi. 16 Akatokeza na vijito gengeni, Akatelemsha maji kama mito. 17 Lakini wakazidi kumtenda dhambi, Walipomwasi Aliye juu katika nchi ya kiu. 18 Wakamjaribu Mungu mioyoni mwao Kwa kutaka chakula kwa tamaa zao. 19 Naam, walimwamba Mungu, wakasema, Je! Mungu aweza kuandika meza jangwani? 20 Tazama, aliupiga mwamba; Maji yakabubujika, ikafurika mito. Pia aweza kutupa chakula? Atawaandalia watu wake nyama? 21 Hivyo Bwana aliposikia akaghadhibika; Moto ukawashwa juu ya Yakobo, Hasira nayo ikapanda juu ya Israeli. 22 Kwa kuwa hawakumwamini Mungu, Wala hawakuutumainia wokovu wake. 23 Lakini aliyaamuru mawingu juu; Akaifungua milango ya mbinguni; 24 Akawanyeshea mana ili wale; Akawapa nafaka ya mbinguni. 25 Mwanadamu akala chakula cha mashujaa; Aliwapelekea chakula cha kuwashibisha. 26 Aliuelekeza upepo wa mashariki mbinguni; Akaiongoza kusi kwa uweza wake. 27 Akawanyeshea nyama kama mavumbi, Na ndege wenye mbawa, Kama mchanga wa bahari. 28 Akawaangusha kati ya matuo yao, Pande zote za maskani zao. 29 Wakala wakashiba sana; Maana aliwaletea walivyovitamani; 30 Hawakuachana na matakwa yao. Ila chakula chao kikali ki vinywani mwao 31 Hasira ya Mungu ikapanda juu yao, Akawaua waliokuwa wanono; Akawaangusha chini vijana wa Israeli. 32 Pamoja na hayo wakazidi kutenda dhambi, Wala hawakuyaamini matendo yake ya ajabu. 33 Kwa hiyo akazikomesha siku zao kama pumzi, Na miaka yao kwa hofu ya kuwasitusha. 34 Alipowaua ndipo walipokuwa wakimtafuta; Wakarudi wakamtaka Mungu kwa bidii. 35 Wakakumbuka kuwa Mungu ni mwamba wao, Na Mungu Aliye juu ni mkombozi wao. 36 Lakini walimdanganya kwa vinywa vyao, Wakamwambia uongo kwa ndimi zao. 37 Kwa maana mioyo yao haikuwa thabiti kwake, Wala hawakuwa waaminifu katika agano lake. 38 Lakini Yeye, kwa kuwa anayo rehema, Husamehe uovu wala haangamizi. Mara nyingi huipishia mbali ghadhabu yake, Wala haiwashi hasira yake yote. 39 Akakumbuka ya kuwa wao ni kiwiliwili, Upepo upitao wala haurudi. 40 Walimwasi jangwani mara ngapi? Na kumhuzunisha nyikani! 41 Wakarudi nyuma wakamjaribu Mungu; Wakampa mpaka Mtakatifu wa Israeli. 42 Hawakuukumbuka mkono wake, Wala siku ile alipowakomboa na mtesi. 43 Alivyoziweka ishara zake katika Misri, Na miujiza yake katika konde la Soani. 44 Aligeuza damu mito yao, Na vijito wasipate kunywa. 45 Aliwapelekea mainzi wakawala, Na vyura wakawaharibu. 46 Akawapa tunutu mazao yao, Na nzige kazi yao. 47 Aliiharibu mizabibu yao kwa mvua ya mawe, Na mikuyu yao kwa mawe ya barafu. 48 Akaacha ng'ombe zao wapigwe kwa mvua ya mawe, Na makundi yao kwa umeme. 49 Akawapelekea ukali wa hasira yake, Ghadhabu, na uchungu, na taabu, Kundi la malaika waletao mabaya. 50 Akiifanyizia njia hasira yake; Wala hakuziepusha roho zao na mauti, Bali aliiachia tauni uhai wao; 51 Akampiga kila mzaliwa wa kwanza wa Misri, Malimbuko ya nguvu katika hema za Hamu. 52 Bali aliwaongoza watu wake kama kondoo, Akawachunga kama kundi jangwani. 53 Hao akawachukua salama wala hawakuogopa, Bali bahari iliwafunikiza adui zao. 54 Akawapeleka hadi mpaka wake mtakatifu, Mlima alioununua kwa mkono wake wa kuume. 55 Akawafukuza mataifa mbele yao, Akawapimia urithi kwa kamba, Na kuwakalisha kabila za Israeli katika hema zao. 56 Lakini walimjaribu Mungu Aliye juu, wakamwasi, Wala hawakuzishika shuhuda zake. 57 Bali walirudi nyuma, wakahaini kama baba zao; Wakaepea kama upinde usiofaa. 58 Wakamkasirisha kwa mahali pao pa juu, Wakamtia wivu kwa sanamu zao. 59 Mungu akasikia, akaghadhibika, Akamkataa Israeli kabisa. 60 Akaiacha maskani ya Shilo, Hema aliyoiweka katikati ya wanadamu; 61 Akaziacha nguvu zake kutekwa, Na fahari yake mkononi mwa mtesi. 62 Akawatoa watu wake wapigwe kwa upanga; Akaughadhibikia urithi wake. 63 Moto ukawala vijana wao, Wanawali wao hawakuimbiwa nyimbo za arusi, 64 Makuhani wao walianguka kwa upanga, Wala wajane wao hawakuomboleza. 65 Ndipo Bwana alipoamka kama aliyelala usingizi, Kama shujaa apigaye kelele sababu ya mvinyo; 66 Akawapiga watesi wake akawarudisha nyuma, Akawatia aibu ya milele. 67 Ila akaikataa hema ya Yusufu; Wala hakuichagua kabila ya Efraimu. 68 Bali aliichagua kabila ya Yuda, Mlima Sayuni alioupenda. 69 Akajenga patakatifu pake kama vilele, Kama dunia aliyoiweka imara milele. 70 Akamchagua Daudi, mtumishi wake, Akamwondoa katika mazizi ya kondoo. 71 Nyuma ya kondoo wanyonyeshao alimwondoa, Awachunge Yakobo watu wake, na Israeli urithi wake. 72 Akawalisha kwa ukamilifu wa moyo wake, Na kuwaongoza kwa busara ya mikono yake.

Zaburi 79

1 Ee Mungu, mataifa wameingia katika urithi wako, Wamelinajisi hekalu lako takatifu. Wamefanya Yerusalemu chungu chungu. 2 Wameziacha maiti za watumishi wako Ziwe chakula cha ndege wa angani. Na miili ya watauwa wako Iwe chakula cha wanyama wa nchi. 3 Wamemwaga damu yao kama maji Pande zote za Yerusalemu, Wala hapakuwa na mzishi. 4 Tumekuwa lawama kwa jirani zetu, Mzaha na dhihaka kwao wanaotuzunguka. 5 Ee Bwana, hata lini? Utaona hasira milele? Wivu wako utawaka kama moto? 6 Ukali wako uwamwagie mataifa wasiokujua, Na falme za hao wasioliitia jina lako. 7 Kwa maana wamemla Yakobo, Na matuo yake wameyaharibu. 8 Usikumbuke juu yetu maovu ya baba zetu, Rehema zako zije kutulaki hima, Kwa maana tumedhilika sana. 9 Ee Mungu wa wokovu wetu, utusaidie, Kwa ajili ya utukufu wa jina lako. Utuokoe, utughofiri dhambi zetu, Kwa ajili ya jina lako. 10 Kwa nini mataifa kusema, Yuko wapi Mungu wao? Kisasi cha damu ya watumishi wako iliyomwagika Kijulike kati ya mataifa machoni petu. 11 Kuugua kwake aliyefungwa Na kuingie mbele zako. Kwa kadiri ya uweza wa mkono wako Uwahifadhi wana wa mauti. 12 Uwalipe jirani zetu mara saba vifuani mwao Laumu zao walizokulaumu, Ee Bwana. 13 Na sisi tulio watu wako, Na kondoo za malisho yako, Tutakushukuru milele; Tutazisimulia sifa zako kizazi kwa kizazi.

Zaburi 80

1 Wewe uchungaye Israeli, usikie, Wewe umwongozaye Yusufu kama kundi; Wewe uketiye juu ya makerubi, utoe nuru. 2 Mbele ya Efraimu, na Benyamini, na Manase, Uziamshe nguvu zako, Uje, utuokoe. 3 Ee Mungu, uturudishe, Uangazishe uso wako nasi tutaokoka. 4 Ee Bwana, Mungu wa majeshi, hata lini Utayaghadhibikia maombi ya watu wako? 5 Umewalisha mkate wa machozi, Umewanywesha machozi kwa kipimo kikuu. 6 Unatufanya sababu ya ugomvi kwa jirani zetu, Na adui zetu wanacheka wao kwa wao. 7 Ee Mungu wa majeshi, uturudishe, Uangazishe uso wako nasi tutaokoka. 8 Ulileta mzabibu kutoka Misri, Ukawafukuza mataifa ukaupanda. 9 Ulitengeneza nafasi mbele yake, Nao ukatia mizizi sana ukaijaza nchi. 10 Milima ilifunikwa kwa uvuli wake, Matawi yake ni kama mierezi ya Mungu. 11 Nao uliyaeneza matawi yake hata baharini, Na vichipukizi vyake hata kunako Mto. 12 Kwa nini umezibomoa kuta zake, Wakauchuma wote wapitao njiani? 13 Nguruwe wa msituni wanauharibu, Na hayawani wa kondeni wanautafuna. 14 Ee Mungu wa majeshi, tunakusihi, urudi, Utazame toka juu uone, uujilie mzabibu huu. 15 Na mche ule ulioupanda Kwa mkono wako wa kuume; Na tawi lile ulilolifanya Kuwa imara kwa nafsi yako. 16 Umechomwa moto; umekatwa; Kwa lawama ya uso wako wanapotea. 17 Mkono wako na uwe juu yake Mtu wa mkono wako wa kuume; Juu ya mwanadamu uliyemfanya Kuwa imara kwa nafsi yako; 18 Basi hatutakuacha kwa kurudi nyuma; Utuhuishe nasi tutaliitia jina lako. 19 Ee Bwana, Mungu wa majeshi, uturudishe, Uangazishe uso wako nasi tutaokoka.

Zaburi 81

1 Mwimbieni Mungu, nguvu zetu, nyimbo za furaha, Mshangilieni Mungu wa Yakobo. 2 Pazeni zaburi, pigeni matari, Kinubi chenye sauti nzuri, na kinanda. 3 Pigeni panda mwandamo wa mwezi, Wakati wa mbalamwezi, sikukuu yetu. 4 Kwa maana ni sheria kwa Israeli, Ni hukumu ya Mungu wa Yakobo. 5 Aliamuru iwe ushuhuda katika Yusufu, Alipoondoka juu ya nchi ya Misri; Maneno yake nisiyemjua naliyasikia. 6 Nimelitenga bega lake na mzigo, Mikono yake ikaachana na kikapu. 7 Katika shida uliniita nikakuokoa; Nalikuitikia katika sitara ya radi; Nalikujaribu penye maji ya Meriba. 8 Enyi watu wangu, sikieni, nami nitawaonya, Ee Israeli, kama ukitaka kunisikiliza; 9 Usiwe na mungu mgeni ndani yako; Wala usimsujudie mungu mwingine. 10 Mimi ndimi Bwana, Mungu wako, Niliyekupandisha toka nchi ya Misri; Fumbua sana kinywa chako nami nitakijaza. 11 Lakini watu wangu hawakuisikiliza sauti yangu, Wala Israeli hawakunitaka. 12 Nikawaacha wakaenda kwa ukaidi wa mioyo yao, Waenende katika mashauri yao. 13 Laiti watu wangu wangenisikiliza, Na Israeli angeenenda katika njia zangu; 14 Ningewadhili adui zao kwa upesi, Na juu ya watesi wao ningegeuza mkono wangu; 15 Wamchukiao Bwana wangenyenyekea mbele zake, Bali wakati wao ungedumu milele.

Zaburi 82

1 Mungu asimama katika kusanyiko la Mungu; Katikati ya miungu anahukumu. 2 Hata lini mtahukumu kwa dhuluma, Na kuzikubali nyuso za wabaya? 3 Mfanyieni hukumu maskini na yatima; Mtendeeni haki aliyeonewa na fukara; 4 Mwokoeni maskini na mhitaji; Mwopoeni mikononi mwa wadhalimu. 5 Hawajui wala hawafahamu, hutembea gizani; Misingi yote ya nchi imetikisika. 6 Mimi nimesema, Ndinyi miungu, Na wana wa Aliye juu, nyote pia. 7 Lakini mtakufa kama wanadamu, Mtaanguka kama mmoja wa wakuu. 8 Ee Mungu, usimame, uihukumu nchi, Maana Wewe utawarithi mataifa yote.

Zaburi 83

1 Ee Mungu, usistarehe, Ee Mungu, usinyamae, wala usitulie. 2 Maana adui zako wanafanya ghasia, Nao wakuchukiao wameviinua vichwa vyao. 3 Juu ya watu wako wanafanya hila, Na kushauriana juu yao uliowaficha. 4 Wamesema, Njoni, tuwakatilie mbali wasiwe taifa, Na jina la Israeli halitakumbukwa tena. 5 Maana wanashauriana kwa moyo mmoja, Juu yako wanafanyana agano. 6 Hema za Edomu, na Waishmaeli, Na Moabu, na Wahagari, 7 Gebali, na Amoni, na Amaleki, Na Filisti, nao wanaokaa Tiro, 8 Ashuri naye amepatana nao, Wamewasaidia wana wa Lutu. 9 Uwatende kama Midiani, kama Sisera, Kama Yabini, penye kijito Kishoni. 10 Ambao waliangamizwa Endori; Wakawa samadi juu ya nchi. 11 Uwafanye wakuu wao kama Orebu na Zeebu, Na masheki yao wote kama Zeba na Zalmuna. 12 Ambao Walisema, Na tutamalaki makao ya Mungu. 13 Ee Mungu, uwafanye kama mavumbi ya kisulisuli, Mithili ya makapi mbele ya upepo, 14 Kama moto uteketezao msitu, Kama miali ya moto iiwashayo milima, 15 Ndivyo utakavyowafuatia kwa tufani yako, Na kuwafadhaisha kwa dhoruba yako. 16 Uwajaze nyuso zao fedheha; Wakalitafute jina lako, Bwana. 17 Waaibike, wafadhaike milele, Naam, watahayarike na kupotea. 18 Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, Ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.

Zaburi 84

1 Maskani zako zapendeza kama nini, Ee Bwana wa majeshi! 2 Nafsi yangu imezionea shauku nyua za Bwana, Naam, na kuzikondea. Moyo wangu na mwili wangu Vinamlilia Mungu aliye hai. 3 Shomoro naye ameona nyumba, Na mbayuwayu amejipatia kioto, Alipoweka makinda yake, Kwenye madhabahu zako, Ee Bwana wa majeshi, Mfalme wangu na Mungu wangu. 4 Heri wakaao nyumbani mwako, Wanakuhimidi daima. 5 Heri ambaye nguvu zake zatoka kwako, Na njia ziendazo Sayuni zimo moyoni mwake. 6 Wakipita kati ya bonde la Vilio, Hulifanya kuwa chemchemi, Naam, mvua ya vuli hulivika baraka 7 Huendelea toka nguvu hata nguvu, Huonekana Sayuni kila mmoja mbele za Mungu. 8 Bwana, Mungu wa majeshi, uyasikie maombi yangu, Ee Mungu wa Yakobo, usikilize, 9 Ee Mungu, ngao yetu, uangalie, Umtazame uso masihi wako. 10 Hakika siku moja katika nyua zako Ni bora kuliko siku elfu. Ningependa kuwa bawabu nyumbani mwa Mungu wangu, Kuliko kukaa katika hema za uovu. 11 Kwa kuwa Bwana, Mungu, ni jua na ngao, Bwana atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema Hao waendao kwa ukamilifu. 12 Ee Bwana wa majeshi, Heri mwanadamu anayekutumaini Wewe.

Zaburi 85

1 Bwana, umeiridhia nchi yako, Umewarejeza mateka wa Yakobo. 2 Umeusamehe uovu wa watu wako, Umezisitiri hatia zao zote. 3 Umeiondoa ghadhabu yako yote, Umerudi na kuuacha ukali wa hasira yako. 4 Mungu wa wokovu wetu, uturudishe, Uikomeshe hasira uliyo nayo juu yetu. 5 Je! Utatufanyia hasira hata milele? Utadumisha ghadhabu kizazi hata kizazi? 6 Je! Hutaki kurudi na kutuhuisha, Watu wako wakufurahie? 7 Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako, Utupe wokovu wako. 8 Na nisikie atakavyosema Mungu Bwana, Maana atawaambia watu wake amani, Naam, na watauwa wake pia, Bali wasiurudie upumbavu tena. 9 Hakika wokovu wake u karibu na wamchao, Utukufu ukae katika nchi yetu. 10 Fadhili na kweli zimekutana, Haki na amani zimehusiana. 11 Kweli imechipuka katika nchi, Haki imechungulia kutoka mbinguni. 12 Naam, Bwana atatoa kilicho chema, Na nchi yetu itatoa mazao yake. 13 Haki itakwenda mbele zake, Nayo itazifanya hatua zake kuwa njia.

Zaburi 86

1 Ee Bwana, utege sikio lako unijibu, Maana mimi ni maskini na mhitaji 2 Unihifadhi nafsi yangu, Maana mimi ni mcha Mungu. Wewe uliye Mungu wangu, Umwokoe mtumishi wako anayekutumaini. 3 Wewe, Bwana, unifadhili, Maana nakulilia Wewe mchana kutwa. 4 Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako, Maana nafsi yangu nakuinulia Wewe, Bwana. 5 Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema, Umekuwa tayari kusamehe, Na mwingi wa fadhili, Kwa watu wote wakuitao. 6 Ee Bwana, uyasikie maombi yangu; Uisikilize sauti ya dua zangu. 7 Siku ya mateso yangu nitakuita, Kwa maana utaniitikia. 8 Katikati ya miungu hakuna kama Wewe, Bwana, Wala matendo mfano wa matendo yako. 9 Mataifa yote uliowafanya watakuja; Watakusujudia Wewe, Bwana, Watalitukuza jina lako; 10 Kwa kuwa ndiwe uliye mkuu, Wewe ndiwe mfanya miujiza, Ndiwe Mungu peke yako. 11 Ee Bwana, unifundishe njia yako; Nitakwenda katika kweli yako; Moyo wangu na ufurahi kulicha jina lako; 12 Nitakusifu Wewe, Bwana, Mungu wangu, Kwa moyo wangu wote, Nitalitukuza jina lako milele. 13 Maana fadhili zako kwangu ni nyingi sana; Umeiopoa nafsi yangu na kuzimu. 14 Ee Mungu, wenye kiburi wamenishambulia; Mkutano wa wakatili wamenitafuta roho. Wala hawakukuweka Wewe Mbele ya macho yao. 15 Lakini Wewe, Bwana, U Mungu wa rehema na neema, Mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli. 16 Unielekee na kunifadhili mimi; Mpe mtumishi wako nguvu zako, Umwokoe mwana wa mjakazi wako. 17 Unifanyie ishara ya wema, Wanichukiao waione na kuaibishwa. Kwa kuwa Wewe, Bwana, Umenisaidia na kunifariji.

Zaburi 87

1 Msingi wake upo Juu ya milima mitakatifu. 2 Bwana ayapenda malango ya Sayuni Kuliko maskani zote za Yakobo. 3 Umetajwa kwa mambo matukufu, Ee Mji wa Mungu. 4 Nitataja Rahabu na Babeli Miongoni mwao wanaonijua. Tazama Filisti, na Tiro, na Kushi; Huyu alizaliwa humo. 5 Naam, mintarafu Sayuni itasemwa, Huyu na huyu alizaliwa humo. Na Yeye Aliye juu Ataufanya imara. 6 Bwana atahesabu, awaandikapo mataifa, Huyu alizaliwa humo. 7 Waimbao na wachezao na waseme, Visima vyangu vyote vimo mwako.

Zaburi 88

1 Ee Bwana, Mungu wa wokovu wangu Mchana na usiku nimelia mbele zako. 2 Maombi yangu yafike mbele zako, Uutegee ukelele wangu sikio lako. 3 Maana nafsi yangu imeshiba taabu, Na uhai wangu umekaribia kuzimu. 4 Nimehesabiwa pamoja nao washukao shimoni; Nimekuwa kama mtu asiye na msaada. 5 Miongoni mwao waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako. 6 Mimi umenilaza katika shimo la chini, Katika mahali penye giza vilindini. 7 Ghadhabu yako imenilemea, Umenitesa kwa mawimbi yako yote. 8 Wanijuao umewatenga nami; Umenifanya kuwa chukizo kwao; Nimefungwa wala siwezi kutoka. 9 Jicho langu limefifia kwa ajili ya mateso Bwana, nimekuita kila siku; Nimekunyoshea Wewe mikono yangu. 10 Wafu je! Utawafanyia miujiza? Au waliofariki watasimama na kukuhimidi? 11 Fadhili zako zitasimuliwa kaburini? Au uaminifu wako katika uharibifu? 12 Miujiza yako itajulikana gizani? Au haki yako katika nchi ya usahaulifu? 13 Lakini mimi nimekulilia Wewe, Bwana, Na asubuhi maombi yangu yatakuwasilia. 14 Bwana, kwa nini kuitupa nafsi yangu, Na kunificha uso wako? 15 Nateswa mimi hali ya kufa tangu ujana, Nimevumilia vitisho vyako na kufadhaika. 16 Hasira zako kali zimepita juu yangu, Maogofyo yako yameniangamiza. 17 Yamenizunguka kama maji mchana kutwa, Yamenisonga yote pamoja. 18 Mpenzi na rafiki umewatenga nami, Nao wanijuao wamo gizani.

Zaburi 89

1 Fadhili za Bwana nitaziimba milele; Kwa kinywa changu nitavijulisha vizazi vyote uaminifu wako. 2 Maana nimesema, Fadhili zitajengwa milele; Katika mbingu utauthibitisha uaminifu wako. 3 Nimefanya agano na mteule wangu, Nimemuapia Daudi, mtumishi wangu. 4 Wazao wako nitawafanya imara milele, Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. 5 Ee Bwana, mbingu zitayasifu maajabu yako, Uaminifu wako katika kusanyiko la watakatifu. 6 Maana ni nani katika mbingu awezaye kulinganishwa na Bwana? Ni nani afananaye na Bwana miongoni mwa malaika? 7 Mungu huogopwa sana barazani pa watakatifu, Ni wa kuhofiwa kuliko wote wanaomzunguka. 8 Bwana, Mungu wa majeshi, Ni nani aliye hodari kama Wewe, Ee YAHU? Na uaminifu wako unakuzunguka. 9 Wewe ndiwe ukitawalaye kiburi cha bahari. Mawimbi yake yainukapo wayatuliza Wewe. 10 Ndiwe uliyemseta Rahabu akawa kama aliyeuawa, Kwa mkono hodari umewatawanya wakuchukiao. 11 Mbingu ni mali yako, nchi nayo ni mali yako, Ulimwengu na vyote viujazavyo Ndiwe uliyeupiga msingi wake. 12 Kaskazini na kusini ndiwe uliyeziumba, Tabori na Hermoni hulifurahia jina lako. 13 Mkono wako ni mkono wenye uweza, Mkono wako una nguvu, Mkono wako wa kuume umetukuka. 14 Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chako, Fadhili na kweli zahudhuria mbele za uso wako. 15 Heri watu wale waijuao sauti ya shangwe, Ee Bwana, huenenda katika nuru ya uso wako. 16 Kwa jina lako hufurahi mchana kutwa, Na kwa haki yako hutukuzwa. 17 Maana fahari ya nguvu zao ni Wewe, Na kwa radhi yako pembe yetu itatukuka. 18 Maana ngao yetu ina Bwana, Na mfalme wetu ni wake Mtakatifu wa Israeli. 19 Ndipo ulipowaambia watakatifu wako kwa njozi, Ukasema, nimempa aliye hodari msaada; Nimemtukuza aliyechaguliwa miongoni mwa watu. 20 Nimemwona Daudi, mtumishi wangu, Nimempaka mafuta yangu matakatifu. 21 Ambaye mkono wangu utakuwa thabiti kwake, Na mkono wangu utamtia nguvu. 22 Adui hatamwonea, Wala mwana wa uovu hatamtesa. 23 Bali nitawaponda watesi wake mbele yake, Nitawapiga wanaomchukia. 24 Uaminifu wangu na fadhili zangu atakuwa nazo, Na kwa jina langu pembe yake itatukuka. 25 Nitaweka mkono wake juu ya bahari, Na mkono wake wa kuume juu ya mito. 26 Yeye ataniita, Wewe baba yangu, Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu. 27 Nami nitamjalia kuwa mzaliwa wangu wa kwanza, Kuwa juu sana kuliko wafalme wa dunia. 28 Hata milele nitamwekea fadhili zangu, Na agano langu litafanyika amini kwake. 29 Wazao wake nao nitawadumisha milele, Na kiti chake cha enzi kama siku za mbingu. 30 Wanawe wakiiacha sheria yangu, Wasiende katika hukumu zangu, 31 Wakizihalifu amri zangu, Wasiyashike maagizo yangu, 32 Basi, nitawarudi makosa yao kwa fimbo, Na uovu wao kwa mapigo. 33 Lakini fadhili zangu sitamwondolea yeye, Wala sitafanya uaminifu wangu kuwa uongo. 34 Mimi sitalihalifu agano langu, Sitalibadili neno lililotoka midomoni mwangu. 35 Neno moja nimeliapa kwa utakatifu wangu, Hakika sitamwambia Daudi uongo, 36 Wazao wake watadumu milele, Na kiti chake kitakuwa kama jua mbele zangu. 37 Kitathibitika milele kama mwezi; Shahidi aliye mbinguni mwaminifu. 38 Walakini Wewe umemtupa na kumkataa, Umemghadhibikia masihi wako. 39 Umechukizwa na agano la mtumishi wako, Umeinajisi taji yake na kuitupa chini. 40 Umeyabomoa maboma yake yote, Umezifanya ngome zake kuwa magofu. 41 Wote wapitao njiani wanateka mali zake; Amekuwa laumu kwa jirani zake; 42 Umeutukuza mkono wa kuume wa watesi wake; Umewafurahisha wote wanaomchukia. 43 Pia umeurudisha nyuma ukali wa upanga wake; Wala hukumsimamisha vitani. 44 Umeikomesha fahari yake; Kiti chake cha enzi umekitupa chini. 45 Umezipunguza siku za ujana wake; Umemvika aibu. 46 Ee Bwana, hata lini? Utajificha hata milele? Ghadhabu yako itawaka kama moto? 47 Ukumbuke jinsi mimi nisivyo wa kudumu; Kwa ubatili gani umeiumba jamii ya wanadamu! 48 Ni mwanamume gani atakayeishi asione mauti, Atakayejiokoa nafsi yake na mkono wa kuzimu? 49 Bwana, zi wapi fadhili zako za kwanza, Ulizomwapia Daudi kwa uaminifu wako? 50 Ee Bwana, ukumbuke, Wanavyosimangwa watumishi wako; Jinsi ninavyostahimili kifuani mwangu Masimango ya watu wengi. 51 Ambayo adui zako wamesimanga, Ee Bwana, Naam, wamezisimanga hatua za masihi wako. 52 Na ahimidiwe Bwana milele. Amina na Amina.

Zaburi 90

1 Wewe, Bwana, umekuwa makao yetu, Kizazi baada ya kizazi. 2 Kabla haijazaliwa milima, wala hujaiumba dunia, Na tangu milele hata milele ndiwe Mungu. 3 Wamrudisha mtu mavumbini, usemapo, Rudini, enyi wanadamu. 4 Maana miaka elfu machoni pako Ni kama siku ya jana ikiisha kupita, Na kama kesha la usiku. 5 Wawagharikisha, huwa kama usingizi, Asubuhi huwa kama majani yameayo. 6 Asubuhi yachipuka na kumea, Jioni yakatika na kukauka. 7 Maana tumetoweshwa kwa hasira yako, Na kwa ghadhabu yako tumefadhaishwa. 8 Umeyaweka maovu yetu mbele zako, Siri zetu katika mwanga wa uso wako. 9 Maana siku zetu zote zimepita katika hasira yako, Tumetowesha miaka yetu kama kite. 10 Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara. 11 Ni nani aujuaye uweza wa hasira yako? Na ghadhabu yako kama ipasavyo kicho chako? 12 Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, Tujipatie moyo wa hekima. 13 Ee Bwana urudi, hata lini? Uwahurumie watumishi wako. 14 Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako, Nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote. 15 Utufurahishe kwa kadiri ya siku ulizotutesa, Kama miaka ile tuliyoona mabaya. 16 Matendo yako na yaonekane kwa watumishi wako, Na adhama yako kwa watoto wao. 17 Na uzuri wa Bwana, Mungu wetu, uwe juu yetu, Na kazi ya mikono yetu utufanyie thabiti, Naam, kazi ya mikono yetu uithibitishe.

Zaburi 91

1 Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. 2 Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. 3 Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, Na katika tauni iharibuyo. 4 Kwa manyoya yake atakufunika, Chini ya mbawa zake utapata kimbilio; Uaminifu wake ni ngao na kigao. 5 Hutaogopa hofu ya usiku, Wala mshale urukao mchana, 6 Wala tauni ipitayo gizani, Wala uele uharibuo adhuhuri, 7 Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. 8 Ila kwa macho yako utatazama, Na kuyaona malipo ya wasio haki. 9 Kwa kuwa Wewe Bwana ndiwe kimbilio langu; Umemfanya Aliye juu kuwa makao yako. 10 Mabaya hayatakupata wewe, Wala tauni haitaikaribia hema yako. 11 Kwa kuwa atakuagizia malaika zake Wakulinde katika njia zako zote. 12 Mikononi mwao watakuchukua, Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe. 13 Utawakanyaga simba na nyoka, Mwana-simba na joka utawaseta kwa miguu. 14 Kwa kuwa amekaza kunipenda Nitamwokoa; na kumweka palipo juu, Kwa kuwa amenijua Jina langu. 15 Ataniita nami nitamwitikia; Nitakuwa pamoja naye taabuni, Nitamwokoa na kumtukuza; 16 Kwa siku nyingi nitamshibisha, Nami nitamwonyesha wokovu wangu.

Zaburi 92

1 Ni neno jema kumshukuru Bwana, Na kuliimbia jina lako, Ee Uliye juu. 2 Kuzitangaza rehema zako asubuhi, Na uaminifu wako wakati wa usiku. 3 Kwa chombo chenye nyuzi kumi, Na kwa kinanda, Na kwa mlio wa kinubi. 4 Kwa kuwa umenifurahisha, Bwana, Kwa kazi yako; nitashangilia Kwa ajili ya matendo ya mikono yako. 5 Ee Bwana, jinsi yalivyo makuu matendo yako! Mawazo yako ni mafumbo makubwa. 6 Mtu mjinga hayatambui hayo, Wala mpumbavu hayafahamu. 7 Wasio haki wakichipuka kama majani Na wote watendao maovu wakistawi. Ni kwa kusudi waangamizwe milele; 8 Bali Wewe, Bwana, U Mtukufu hata milele. 9 Maana hao adui zako, Ee Bwana, Hao adui zako watapotea, Na watendao maovu watatawanyika wote pia. 10 Bali pembe yangu umeiinua kama pembe ya nyati, Nimepakwa mafuta mabichi. 11 Na jicho langu limewatazama walioniotea, Sikio langu limesikia habari za waovu walionishambulia. 12 Mwenye haki atasitawi kama mtende, Atakua kama mwerezi wa Lebanoni. 13 Waliopandwa katika nyumba ya Bwana Watasitawi katika nyua za Mungu wetu. 14 Watazaa matunda hadi wakati wa uzee, Watajaa utomvu, watakuwa na ubichi. 15 Watangaze ya kuwa Bwana ni mwenye adili, Mwamba wangu, ndani yake hamna udhalimu.

Zaburi 93

1 Bwana ametamalaki, amejivika adhama, Bwana amejivika, na kujikaza nguvu. Naam, ulimwengu umethibitika usitikisike; 2 Kiti chako kimekuwa thabiti tokea zamani; Wewe ndiwe uliye tangu milele. 3 Ee Bwana, mito imepaza, Mito imepaza sauti zake, Mito imepaza uvumi wake. 4 Kupita sauti ya maji mengi, maji makuu, Kupita mawimbi ya bahari yaumkayo, Bwana Aliye juu ndiye mwenye ukuu. 5 Shuhuda zako ni amini sana; Utakatifu ndio uifaao nyumba yako, Ee Bwana, milele na milele.

Zaburi 94

1 Ee Bwana, Mungu wa kisasi, Mungu wa kisasi, uangaze, 2 Mwenye kuihukumu nchi, ujitukuze, Uwape wenye kiburi stahili zao. 3 Bwana, hata lini wasio haki, Hata lini wasio haki watashangilia? 4 Je! Wote watendao uovu watatoa maneno, Na kusema majivuno, na kufanya kiburi? 5 Ee Bwana, wanawaseta watu wako; Wanautesa urithi wako; 6 Wanamwua mjane na mgeni; Wanawafisha yatima. 7 Nao husema, Bwana haoni; Mungu wa Yakobo hafikiri. 8 Enyi wajinga miongoni mwa watu, fikirini; Enyi wapumbavu, lini mtakapopata akili? 9 Aliyelitia sikio mahali pake asisikie? Aliyelifanya jicho asione? 10 Awaadibuye mataifa asikemee? Amfundishaye mwanadamu asijue? 11 Bwana anajua mawazo ya mwanadamu, Ya kuwa ni ubatili. 12 Ee Bwana, heri mtu yule umwadibuye, Na kumfundisha kwa sheria yako; 13 Upate kumstarehesha siku za mabaya, Hata asiye haki atakapochimbiwa shimo. 14 Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake, Wala hutauacha urithi wake, 15 Maana hukumu itairejea haki, Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata. 16 Ni nani atakayesimama Kwa ajili yangu juu ya wabaya? Ni nani atakayenisaidia Juu yao wafanyao maovu? 17 Kama Bwana asingalikuwa msaada wangu, Nafsi yangu kwa upesi ingalikaa penye kimya. 18 Niliposema, Mguu wangu unateleza; Ee Bwana, fadhili zako zilinitegemeza. 19 Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, Faraja zako zaifurahisha roho yangu. 20 Je! Kiti cha udhalimu kishirikiane nawe, Kitungacho madhara kwa njia ya sheria? 21 Huishambulia nafsi yake mwenye haki, Na kuihukumu damu isiyo na hatia. 22 Lakini Bwana amekuwa ngome kwangu, Na Mungu wangu mwamba wangu wa kukimbilia.

Zaburi 95

1 Njoni, tumwimbie Bwana, Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu. 2 Tuje mbele zake kwa shukrani, Tumfanyie shangwe kwa zaburi. 3 Kwa kuwa Bwana ni Mungu mkuu, Na Mfalme mkuu juu ya miungu yote. 4 Mkononi mwake zimo bonde za dunia, Hata vilele vya milima ni vyake. 5 Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya, Na mikono yake iliumba nchi kavu. 6 Njoni, tuabudu, tusujudu, Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba. 7 Kwa maana ndiye Mungu wetu, Na sisi tu watu wa malisho yake, Na kondoo za mkono wake. Ingekuwa heri leo msikie sauti yake! 8 Msifanye migumu mioyo yenu; Kama vile huko Meriba Kama siku ya Masa jangwani. 9 Hapo waliponijaribu baba zenu, Wakanipima, wakayaona matendo yangu. 10 Miaka arobaini nalihuzunika na kizazi kile, Nikasema, Hao ni watu waliopotoka mioyo, Hawakuzijua njia zangu. 11 Nikaapa kwa hasira yangu Wasiingie rahani mwangu.

Zaburi 96

1 Mwimbieni Bwana wimbo mpya, Mwimbieni Bwana, nchi yote. 2 Mwimbieni Bwana, libarikini jina lake, Tangazeni wokovu wake siku kwa siku. 3 Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, Na watu wote habari za maajabu yake. 4 Kwa kuwa Bwana ni mkuu mwenye kusifiwa sana. Na wa kuhofiwa kuliko miungu yote. 5 Maana miungu yote ya watu si kitu, Lakini Bwana ndiye aliyezifanya mbingu. 6 Heshima na adhama ziko mbele zake, Nguvu na uzuri zimo katika patakatifu pake. 7 Mpeni Bwana, enyi jamaa za watu, Mpeni Bwana utukufu na nguvu. 8 Mpeni Bwana utukufu wa jina lake, Leteni sadaka mkaziingie nyua zake. 9 Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu, Tetemekeni mbele zake, nchi yote. 10 Semeni katika mataifa, Bwana ametamalaki; Naam, ulimwengu umethibitika usitikisike, Atawahukumu watu kwa adili. 11 Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie, Bahari na ivume na vyote viijazavyo, 12 Mashamba na yashangilie, na vyote vilivyomo, Ndipo miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha; 13 Mbele za Bwana, kwa maana anakuja, Kwa maana anakuja aihukumu nchi. Atauhukumu ulimwengu kwa haki, Na mataifa kwa uaminifu wake.

Zaburi 97

1 Bwana ametamalaki, nchi na ishangilie, Visiwa vingi na vifurahi. 2 Mawingu na giza vyamzunguka, Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chake. 3 Moto hutangulia mbele zake, Nao huwateketeza watesi wake pande zote. 4 Umeme wake uliuangaza ulimwengu, Nchi ikaona ikatetemeka. 5 Milima iliyeyuka kama nta mbele za Bwana, Mbele za Bwana wa dunia yote. 6 Mbingu zimetangaza haki yake, Na watu wote wameuona utukufu wake. 7 Na waaibishwe wote waabuduo sanamu, Wajivunao kwa vitu visivyofaa; Enyi miungu yote, msujuduni Yeye. 8 Sayuni imesikia na kufurahi, Binti za Yuda walishangilia, Kwa sababu ya hukumu zako, Ee Bwana. 9 Maana Wewe, Bwana, ndiwe Uliye juu, Juu sana kuliko nchi yote; Umetukuka sana juu ya miungu yote. 10 Enyi mmpendao Bwana, uchukieni uovu; Huwalinda nafsi zao watauwa wake, Na kuwaokoa na mkono wa wasio haki. 11 Nuru imemzukia mwenye haki, Na furaha wanyofu wa moyo. 12 Enyi wenye haki, mmfurahieni Bwana, Na kulishukuru jina lake takatifu.

Zaburi 98

1 Mwimbieni Bwana wimbo mpya, Kwa maana ametenda mambo ya ajabu. Mkono wa kuume wake mwenyewe, Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu. 2 Bwana ameufunua wokovu wake, Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake. 3 Amezikumbuka rehema zake, Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli. Miisho yote ya dunia imeuona Wokovu wa Mungu wetu. 4 Mshangilieni Bwana, nchi yote, Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. 5 Mwimbieni Bwana zaburi kwa kinubi, Kwa kinubi na sauti ya zaburi. 6 Kwa panda na sauti ya baragumu. Shangilieni mbele za Mfalme, Bwana. 7 Bahari na ivume na vyote viijazavyo, Ulimwengu nao wanaokaa ndani yake. 8 Mito na ipige makofi, Milima na iimbe pamoja kwa furaha. 9 Mbele za Bwana; Kwa maana anakuja aihukumu nchi. Atauhukumu ulimwengu kwa haki, Na mataifa kwa adili.

Zaburi 99

1 Bwana ametamalaki, mataifa wanatetemeka; Ameketi juu ya makerubi, nchi inatikisika. 2 Bwana katika Sayuni ni mkuu, Naye ametukuka juu ya mataifa yote. 3 Na walishukuru jina lake kuu la kuhofiwa; Ndiye mtakatifu. 4 Nguvu za mfalme nazo zapenda hukumu; Wewe ndiwe uliyeithibitisha adili; Ulifanya hukumu na haki katika Yakobo. 5 Mtukuzeni Bwana, Mungu wetu; Sujuduni penye kiti cha miguu yake; Ndiye mtakatifu. 6 Musa na Haruni miongoni mwa makuhani wake, Na Samweli miongoni mwao waliitiao jina lake, Walipomwita Bwana aliwaitikia; 7 Katika nguzo ya wingu alikuwa akisema nao. Walishika shuhuda zake na amri aliyowapa. 8 Ee Bwana, Mungu wetu, ndiwe uliyewajibu; Ulikuwa kwao Mungu mwenye kusamehe Ingawa uliwapatiliza matendo yao. 9 Mtukuzeni Bwana, Mungu wetu; Sujuduni mkiukabili mlima wake mtakatifu; Maana Bwana, Mungu wetu, ndiye mtakatifu.

Zaburi 100

Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote; 2 Mtumikieni Bwana kwa furaha; Njoni mbele zake kwa kuimba; 3 Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu; Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake; Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. 4 Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; Nyuani mwake kwa kusifu; Mshukuruni, lihimidini jina lake;

Zaburi 101

1 Rehema na hukumu nitaziimba, Ee Bwana, nitakuimbia zaburi. 2 Nitaiangalia njia ya unyofu; Utakuja kwangu lini? Nitakwenda kwa unyofu wa moyo Ndani ya nyumba yangu. 3 Sitaweka mbele ya macho yangu Neno la uovu. Kazi yao waliopotoka naichukia, Haitaambatana nami. 4 Moyo wa ukaidi utaondoka kwangu, Lililo ovu sitalijua. 5 Amsingiziaye jirani yake kwa siri, Huyo nitamharibu. Mwenye macho ya kiburi na moyo wa majivuno, Huyo sitavumilia naye. 6 Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi, Hao wakae nami. Yeye aendaye katika njia kamilifu, Ndiye atakayenitumikia. 7 Hatakaa ndani ya nyumba yangu Mtu atendaye hila. Asemaye uongo hatathibitika Mbele ya macho yangu. 8 Asubuhi hata asubuhi nitawaharibu Wabaya wote wa nchi. Niwatenge wote watendao uovu Na mji wa Bwana.

Zaburi 102

1 Ee Bwana, usikie kuomba kwangu, Kilio changu kikufikie. 2 Usinifiche uso wako siku ya shida yangu, Unitegee sikio lako, siku niitapo unijibu upesi. 3 Maana siku zangu zinatoweka kama moshi, Na mifupa yangu inateketea kama kinga. 4 Moyo wangu umepigwa kama majani na kukauka, Naam, ninasahau kula chakula changu. 5 Kwa ajili ya sauti ya kuugua kwangu Mifupa yangu imegandamana na nyama yangu. 6 Nimekuwa kama mwari nyuni wa jangwani, Na kufanana na bundi wa mahameni. 7 Nakesha, tena nimekuwa kama shomoro Aliye peke yake juu ya nyumba. 8 Adui zangu wananilaumu mchana kutwa; Wanaonichukia kana kwamba wana wazimu Huapa kwa kunitaja mimi. 9 Maana nimekula majivu kama chakula, Na kukichanganya kinywaji changu na machozi. 10 Kwa sababu ya ghadhabu yako na hasira yako; Maana umeniinua na kunitupilia mbali. 11 Siku zangu zi kama kivuli kilichotandaa, Nami ninanyauka kama majani. 12 Bali Wewe, Bwana utaketi ukimiliki milele, Na kumbukumbu lako kizazi hata kizazi. 13 Wewe mwenyewe utasimama, Na kuirehemu Sayuni, Kwa maana ndio wakati wa kuihurumia, Naam, majira yaliyoamriwa yamewadia. 14 Maana watumishi wako wameyaridhia mawe yake, Na kuyaonea huruma mavumbi yake. 15 Kisha mataifa wataliogopa jina la Bwana, Na wafalme wote wa dunia utukufu wako; 16 Bwana atakapokuwa ameijenga Sayuni, Atakapoonekana katika utukufu wake, 17 Atakapoyaelekea maombi yake aliye mkiwa, Asiyadharau maombi yao. 18 Kizazi kitakachokuja kitaandikiwa hayo, Na watu watakaoumbwa watamsifu Bwana. 19 Maana ametazama toka patakatifu pake pa juu, Toka mbinguni Bwana ameiangalia nchi, 20 Ili akusikie kuugua kwake aliyefungwa, Na kuwafungua walioandikiwa kufa. 21 Watu walitangaze jina la Bwana katika Sayuni, Na sifa zake katika Yerusalemu, 22 Pindi mataifa watapokusanyika pamoja, Falme nazo ili kumtumikia Bwana. 23 Amezipunguza nguvu zangu njiani; Amezifupisha siku zangu. 24 Nitasema, Ee Mungu wangu, usiniondoe katikati ya siku zangu; Miaka yako ni tangu kizazi hata kizazi. 25 Hapo mwanzo uliutia msingi wa nchi, Na mbingu ni kazi ya mikono yako. 26 Hizi zitaharibika, bali Wewe utadumu Naam, hizi zitachakaa kama nguo; Na kama mavazi utazibadilisha, Nazo zitabadilika. 27 Lakini Wewe U Yeye yule; Na miaka yako haitakoma. 28 Wana wa watumishi wako watakaa, Na wazao wao wataimarishwa mbele zako.

Zaburi 103

1 Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana. Naam, vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake takatifu. 2 Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote. 3 Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, 4 Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema, 5 Aushibisha mema uzee wako, Ujana wako ukarejezwa kama tai; 6 Bwana ndiye afanyaye mambo ya haki, Na hukumu kwa wote wanaoonewa. 7 Alimjulisha Musa njia zake, Wana wa Israeli matendo yake. 8 Bwana amejaa huruma na neema, Haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. 9 Yeye hatateta sikuzote, Wala hatashika hasira yake milele. 10 Hakututenda sawasawa na hatia zetu, Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. 11 Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, Kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao. 12 Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. 13 Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, Ndivyo Bwana anavyowahurumia wamchao. 14 Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, Na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi. 15 Mwanadamu siku zake zi kama majani; Kama ua la kondeni ndivyo asitawivyo. 16 Maana upepo hupita juu yake, kumbe haliko! Na mahali pake hapatalijua tena. 17 Bali fadhili za Bwana zina wamchao Tangu milele hata milele, Na haki yake ina wana wa wana; 18 Maana, wale walishikao agano lake, Na kuyakumbuka maagizo yake ili wayafanye. 19 Bwana ameweka kiti chake cha enzi mbinguni, Na ufalme wake unavitawala vitu vyote. 20 Mhimidini Bwana, enyi malaika zake, Ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, Mkiisikiliza sauti ya neno lake. 21 Mhimidini Bwana, enyi majeshi yake yote, Ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake. 22 Mhimidini Bwana, enyi matendo yake yote, Mahali pote pa milki yake. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana.

Zaburi 104

1 Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana. Wewe, Bwana, Mungu wangu, Umejifanya mkuu sana; Umejivika heshima na adhama. 2 Umejivika nuru kama vazi; Umezitandika mbingu kama pazia; 3 Na kuziweka nguzo za orofa zake majini. Huyafanya mawingu kuwa gari lake, Na kwenda juu ya mabawa ya upepo, 4 Huwafanya malaika zake kuwa pepo, Na watumishi wake kuwa moto wa miali. 5 Uliiweka nchi juu ya misingi yake, Isitikisike milele. 6 Uliifunika kwa vilindi kama kwa vazi, Maji yalikuwa yakisimama juu ya milima. 7 Kwa kukemea kwako yakakimbia, Kwa sauti ya radi yako yakaenda zake kasi, 8 Yakapanda milima, yakatelemka mabondeni, Mpaka mahali ulipoyatengenezea. 9 Umeweka mpaka yasiupite, Wala yasirudi kuifunikiza nchi. 10 Hupeleka chemchemi katika mabonde; Zapita kati ya milima; 11 Zamnywesha kila mnyama wa kondeni; Punda mwitu huzima kiu yao. 12 Kandokando hukaa ndege wa angani; Kati ya matawi hutoa sauti zao. 13 Huinywesha milima toka orofa zake; Nchi imeshiba mazao ya kazi zako. 14 Huyameesha majani kwa makundi, Na maboga kwa matumizi ya mwanadamu; Ili atoe chakula katika nchi, 15 Na divai imfurahishe mtu moyo wake. Aung'aze uso wake kwa mafuta, Na mkate umburudishe mtu moyo wake. 16 Miti ya Bwana nayo imeshiba, Mierezi ya Lebanoni aliyoipanda. 17 Ndimo ndege wafanyamo vitundu vyao, Na korongo, misunobari ni nyumba yake. 18 Milima mirefu ndiko waliko mbuzi wa mwitu, Na magenge ni kimbilio la wibari. 19 Aliufanya mwezi kwa ajili ya nyakati, Jua latambua kuchwa kwake. 20 Wewe hufanya giza, kukawa usiku, Ndipo atambaapo kila mnyama wa mwitu. 21 Wana-simba hunguruma wakitaka mawindo, Ili kutafuta chakula chao kwa Mungu. 22 Jua lachomoza, wanakwenda zao, Na kujilaza mapangoni mwao. 23 Mwanadamu atoka kwenda zake kazini, Na kwenye utumishi wake mpaka jioni. 24 Ee Bwana, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako. 25 Bahari iko kule, kubwa na upana, Ndimo mlimo viendavyo visivyohesabika, Viumbe hai vidogo kwa vikubwa. 26 Ndimo zipitamo merikebu, Ndimo alimo lewiathani uliyemwumba acheze humo. 27 Hao wote wanakungoja Wewe, Uwape chakula chao kwa wakati wake. 28 Wewe huwapa, Wao wanakiokota; Wewe waukunjua mkono wako, Wao wanashiba mema; 29 Wewe wauficha uso wako, Wao wanafadhaika; Waiondoa pumzi yao, wanakufa, Na kuyarudia mavumbi yao, 30 Waipeleka roho yako, wanaumbwa, Nawe waufanya upya uso wa nchi. 31 Utukufu wa Bwana na udumu milele; Bwana na ayafurahie matendo yake. 32 Aitazama nchi, inatetemeka; Aigusa milima, inatoka moshi. 33 Nitamwimbia Bwana maadamu ninaishi; Nitamshangilia Mungu wangu nikiwa hai; 34 Kutafakari kwangu na kuwe kutamu kwake; Mimi nitamfurahia Bwana. 35 Wenye dhambi waangamizwe katika nchi, Watendao ubaya wasiwepo tena. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana.

Zaburi 105

1 Haleluya. Mshukuruni Bwana,liitieni jina ,Wajulisheni watu matendo yake. 2 Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi, Zitafakarini ajabu zake zote. 3 Jisifuni kwa jina lake takatifu, Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana. 4 Mtakeni Bwana na nguvu zake, Utafuteni uso wake sikuzote. 5 Zikumbukeni ajabu zake alizozifanya, Miujiza yake na hukumu za kinywa chake. 6 Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake; Enyi wana wa Yakobo, wateule wake. 7 Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu; Duniani mwote mna hukumu zake. 8 Analikumbuka agano lake milele; Neno lile aliloviamuru vizazi elfu. 9 Agano alilofanya na Ibrahimu, Na uapo wake kwa Isaka. 10 Alilomthibitishia Yakobo liwe amri, Na Israeli liwe agano la milele. 11 Akisema, Nitakupa wewe nchi ya Kanaani, Iwe urithi wenu mliopimiwa. 12 Walipokuwa watu wawezao kuhesabiwa, Naam, watu wachache na wageni ndani yake, 13 Wakatanga-tanga toka taifa hata taifa, Toka ufalme mmoja hata kwa watu wengine. 14 Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. 15 Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu. 16 Akaiita njaa iijilie nchi, Akakiharibu chakula chote walichokitegemea. 17 Alimpeleka mtu mbele yao, Yusufu aliuzwa utumwani. 18 Walimwumiza miguu yake kwa pingu, Akatiwa katika minyororo ya chuma. 19 Hata wakati wa kuwadia neno lake, Ahadi ya Bwana ilimjaribu. 20 Mfalme alituma watu akamfungua, Mkuu wa watu akamwachia. 21 Akamweka kuwa bwana wa nyumba yake, Na mwenye amri juu ya mali zake zote. 22 Awafunge masheki wake kama apendavyo, Na kuwafundisha wazee wake hekima. 23 Israeli naye akaingia Misri, Yakobo akawa mgeni katika nchi ya Hamu. 24 Akawajalia watu wake wazae sana, Akawafanya kuwa hodari kuliko watesi wao. 25 Akawageuza moyo wawachukie watu wake, Wakawatendea hila watumishi wake. 26 Akamtuma Musa, mtumishi wake, Na Haruni ambaye amemchagua. 27 Akaweka mambo ya ishara zake kati yao, Na miujiza katika nchi ya Hamu. 28 Alituma giza, kukafunga giza, Wala hawakuyaasi maneno yake. 29 Aliyageuza maji yao yakawa damu, Akawafisha samaki wao. 30 Nchi yao ilijaa vyura, Vyumbani mwa wafalme wao. 31 Alisema, kukaja makundi ya mainzi, Na chawa mipakani mwao mwote. 32 Badala ya mvua aliwapa mvua ya mawe, Na moto wa miali katika nchi yao. 33 Akaipiga mizabibu yao na mitini yao, Akaivunja miti ya mipaka yao. 34 Alisema, kukaja nzige, Na tunutu wasiohesabika; 35 Wakaila miche yote ya nchi yao, Wakayala matunda ya ardhi yao. 36 Akawapiga wazaliwa wa kwanza katika nchi, Malimbuko ya nguvu zao. 37 Akawatoa hali wana fedha na dhahabu, Katika kabila zao asiwepo mwenye kukwaa. 38 Misri ilifurahi walipoondoka, Maana kwa ajili yao hofu imewaangukia. 39 Alitandaza wingu liwe funiko, Na moto utoe nuru usiku. 40 Walipotaka akaleta kware, Akawashibisha chakula cha mbinguni. 41 Akaufunua mwamba, kukabubujika maji, Yakapita pakavuni kama mto. 42 Maana alilikumbuka neno lake takatifu, Na Ibrahimu, mtumishi wake. 43 Akawatoa watu wake kwa shangwe, Na wateule wake kwa nyimbo za furaha. 44 Akawapa nchi za mataifa, wakairithi kazi ya watu; 45 Ili wazishike amri zake, na kuzitii sheria zake. Haleluya.

Zaburi 106

1 Haleluya. Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele. 2 Nani awezaye kuyanena matendo makuu ya Bwana, Kuzihubiri sifa zake zote? 3 Heri washikao hukumu, Na kutenda haki sikuzote. 4 Ee Bwana, unikumbuke mimi, Kwa kibali uliyo nayo kwa watu wako. Unijilie kwa wokovu wako, 5 Ili niuone wema wa wateule wako. Nipate kuifurahia furaha ya taifa lako, Na kujisifu pamoja na watu wako. 6 Tumetenda dhambi pamoja na baba zetu, Tumetenda maovu, tumefanya ubaya. 7 Baba zetu katika Misri Hawakufikiri matendo yako ya ajabu; Hawakukumbuka wingi wa fadhili zako; Wakaasi penye bahari, bahari ya Shamu. 8 Lakini akawaokoa kwa ajili ya jina lake, Ayadhihirishe matendo yake makuu. 9 Akaikemea bahari ya Shamu ikakauka, Akawaongoza vilindini kana kwamba ni uwanda. 10 Akawaokoa na mkono wa mtu aliyewachukia, Na kuwakomboa na mkono wa adui zao. 11 Maji yakawafunika watesi wao, Hakusalia hata mmoja wao. 12 Ndipo walipoyaamini maneno yake, Waliziimba sifa zake. 13 Wakayasahau matendo yake kwa haraka, Hawakulingojea shauri lake. 14 Bali walitamani sana jangwani, Wakamjaribu Mungu nyikani. 15 Akawapa walichomtaka, Akawakondesha roho zao. 16 Wakamhusudu Musa matuoni, Na Haruni, mtakatifu wa Bwana. 17 Nchi ikapasuka ikammeza Dathani, Ikaufunika mkutano wa Abiramu. 18 Moto ukawaka katika mkutano wao, Miali yake ikawateketeza wabaya. 19 Walifanya ndama huko Horebu, Wakaisujudia sanamu ya kuyeyuka. 20 Wakaubadili utukufu wao Kuwa mfano wa ng'ombe mla majani. 21 Wakamsahau Mungu, mwokozi wao, Aliyetenda makuu katika Misri. 22 Matendo ya ajabu katika nchi ya Hamu, Mambo ya kutisha penye bahari ya Shamu. 23 Akasema ya kuwa atawaangamiza Kama Musa, mteule wake, asingalisimama, Mbele zake kama mahali palipobomoka, Ili aigeuze hasira yake asije akawaharibu. 24 Wakaidharau nchi ile ya kupendeza, Wala hawakuliamini neno lake. 25 Bali wakanung'unika hemani mwao, Wala hawakuisikiliza sauti ya Bwana. 26 Ndipo alipowainulia mkono wake, Ya kuwa atawaangamiza jangwani, 27 Na kuwatawanya wazao wao kati ya mataifa, Na kuwatapanya katika nchi mbali. 28 Wakajiambatiza na Baal-Peori, Wakazila dhabihu za wafu. 29 Wakamkasirisha kwa matendo yao; Tauni ikawashambulia. 30 Ndipo Finehasi akasimama akafanya hukumu; Tauni ikazuiliwa. 31 Akahesabiwa kuwa ana haki Kizazi baada ya kizazi hata milele. 32 Wakamghadhibisha penye maji ya Meriba, Hasara ikampata Musa kwa ajili yao, 33 Kwa sababu waliiasi roho yake, Akasema yasiyofaa kwa midomo yake. 34 Hawakuwaharibu watu wa nchi Kama Bwana alivyowaambia; 35 Bali walijichanganya na mataifa, Wakajifunza matendo yao. 36 Wakazitumikia sanamu zao, Nazo zikawa mtego kwao. 37 Naam, walitoa wana wao na binti zao Kuwa dhabihu kwa mashetani. 38 Wakamwaga damu isiyo na hatia, Damu ya wana wao na binti zao, Waliowatoa dhabihu kwa sanamu za Kanaani; Nchi ikatiwa unajisi kwa damu. 39 Ndivyo walivyotiwa uchafu kwa kazi zao, Wakafanya uasherati kwa matendo yao. 40 Hasira ya Bwana ikawaka juu ya watu wake, Akauchukia urithi wake. 41 Akawatia mikononi mwa mataifa, Nao waliowachukia wakawatawala. 42 Adui zao wakawaonea, Wakatiishwa chini ya mkono wao. 43 Mara nyingi aliwaponya, Bali walikuwa wakimwasi kwa mashauri yao, Wakadhilika katika uovu wao. 44 Lakini aliyaangalia mateso yao, Aliposikia kilio chao. 45 Akawakumbukia agano lake; Akawahurumia kwa wingi wa fadhili zake; 46 Akawajalia kuhurumiwa Na watu wote waliowateka. 47 Ee Bwana, Mungu wetu, utuokoe, Utukusanye kwa kututoa katika mataifa, Tulishukuru jina lako takatifu, Tuzifanyie shangwe sifa zako. 48 Na ahimidiwe Bwana, Mungu wa Israeli, Tangu milele hata milele. Watu wote na waseme, Amina. Haleluya.

Zaburi 107

1 Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele. 2 Na waseme hivi waliokombolewa na Bwana, Wale aliowakomboa na mkono wa mtesi. 3 Akawakusanya kutoka nchi zote, Mashariki na magharibi, kaskazini na kusini. 4 Walitanga-tanga jangwani katika njia ya nyika; Hawakuona mji wa kukaa. 5 Waliona njaa, waliona na kiu, Nafsi yao ilikuwa ikizimia ndani yao. 6 Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. 7 Akawaongoza kwa njia ya kunyoka, Wapate kwenda mpaka mji wa kukaa. 8 Na wamshukuru Bwana, kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu. 9 Maana hushibisha nafsi yenye shauku, Na nafsi yenye njaa huijaza mema. 10 Waliokaa katika giza na uvuli wa mauti, Wamefungwa katika taabu na chuma, 11 Kwa sababu waliyaasi maneno ya Mungu, Wakalidharau shauri lake Aliye juu. 12 Hata akawadhili moyo kwa taabu, Wakajikwaa wala hakuna msaidizi. 13 Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. 14 Aliwatoa katika giza na uvuli wa mauti, Akayavunja mafungo yao. 15 Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu. 16 Maana ameivunja milango ya shaba, Ameyakata mapingo ya chuma. 17 Wapumbavu, kwa sababu ya ukosaji wao, Na kwa sababu ya maovu yao, hujitesa. 18 Nafsi zao zachukia kila namna ya chakula, Wameyakaribia malango ya mauti. 19 Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. 20 Hulituma neno lake, huwaponya, Huwatoa katika maangamizo yao. 21 Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu. 22 Na wamtolee dhabihu za kushukuru, Na kuyasimulia matendo yake kwa kuimba. 23 Washukao baharini katika merikebu, Wafanyao kazi yao katika maji mengi, 24 Hao huziona kazi za Bwana, Na maajabu yake vilindini. 25 Maana husema, akavumisha upepo wa dhoruba, Ukayainua juu mawimbi yake. 26 Wapanda mbinguni, watelemka vilindini, Nafsi yao yayeyuka kwa hali mbaya. 27 Wayumba-yumba, wapepesuka kama mlevi, Akili zao zote zawapotea. 28 Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. 29 Huituliza dhoruba, ikawa shwari, Mawimbi yake yakanyamaza. 30 Ndipo walipofurahi kwa kuwa yametulia Naye huwaleta mpaka bandari waliyoitamani. 31 Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu. 32 Na wamtukuze katika kusanyiko la watu, Na wamhimidi katika baraza ya wazee. 33 Amegeuza mito ikawa jangwa, Na chemchemi za maji zikawa nchi ya kiu. 34 Nchi ya matunda mengi ikawa uwanda wa chumvi, Kwa sababu ya ubaya wao walioikaa. 35 Amegeuza jangwa ikawa ziwa la maji, Na nchi kavu ikawa chemchemi za maji. 36 Maana amewakalisha huko wenye njaa, Nao wametengeneza mji wa kukaa. 37 Wakapanda mbegu katika mashamba, Na kutia mizabibu iliyotoa matunda yake. 38 Naye huwabariki wakaongezeka sana, Wala hayapunguzi makundi yao. 39 Kisha wakapungua na kudhilika, Kwa kuonewa na mabaya na huzuni. 40 Akawamwagia wakuu dharau, Na kuwazungusha katika nyika isiyo na njia. 41 Akamweka mhitaji juu mbali na mateso, Akamfanyia jamaa kama kundi la kondoo. 42 Wanyofu wa moyo wataona na kufurahi, Na uovu wa kila namna utajifumba kinywa. 43 Aliye na hekima na ayaangalie hayo; Na wazitafakari fadhili za Bwana.

Zaburi 108

1 Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Nitaimba, nitaimba zaburi, Naam, kwa utukufu wangu. 2 Amka, kinanda na kinubi, Nitaamka alfajiri. 3 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, Nitakuimbia zaburi kati ya mataifa. 4 Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni. 5 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako. 6 Ili wapenzi wako waopolewe, Uokoe kwa mkono wako wa kuume, uniitikie. 7 Mungu amenena kwa utakatifu wake, Nami nitashangilia. Nitaigawanya Shekemu, Nitalipima bonde la Sukothi. 8 Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu, Na Efraimu ni nguvu ya kichwa changu. Yuda ni fimbo yangu ya kifalme, 9 Moabu ni bakuli langu la kunawia. Nitamtupia Edomu kiatu changu, Na kumpigia Filisti kelele za vita. 10 Ni nani atakayenipeleka hata mji wenye boma? Ni nani atakayeniongoza hata Edomu? 11 Ee Mungu, si Wewe uliyetutupa? Wala, Ee Mungu, hutoki na majeshi yetu? 12 Utuletee msaada juu ya mtesi, Maana wokovu wa binadamu haufai. 13 Kwa msaada wa Mungu tutatenda makuu, Maana Yeye atawakanyaga watesi wetu.

Zaburi 109

1 Ee Mungu wa sifa zangu, usinyamaze, 2 Kwa maana wamenifumbulia kinywa; Kinywa cha mtu asiye haki, cha hila, Wamesema nami kwa ulimi wa uongo. 3 Naam, kwa maneno ya chuki wamenizunguka, Wamepigana nami bure. 4 Badala ya upendo wangu wao hunishitaki, Ijapokuwa naliwaombea. 5 Wamenichukuza mabaya badala ya mema, Na chuki badala ya upendo wangu. 6 Uweke mtu mkorofi juu yake, Mshitaki asimame mkono wake wa kuume. 7 Katika kuhukumiwa ataonekana hana haki, Na sala yake itadhaniwa kuwa ni dhambi. 8 Siku zake na ziwe chache, Usimamizi wake na atwae mtu mwingine. 9 Wanawe na wawe yatima, Na mkewe na awe mjane. 10 Kutanga na watange wanawe na kuomba, Watafute chakula mbali na mahame yao. 11 Mdai na anase vitu vyote alivyo navyo, Wageni na wateke mapato ya kazi yake. 12 Asiwe na mtu wa kumfanyia fadhili, Wala mtu wa kuwahurumia yatima wake. 13 Wazao wake waangamizwe, Jina lao likafutwe katika kizazi cha pili. 14 Uovu wa baba zake ukumbukwe mbele za Bwana, Na dhambi ya mamaye isifutwe. 15 Ziwe mbele za Bwana daima, Aliondoe kumbukumbu lao duniani. 16 Kwa kuwa hakukumbuka kutenda fadhili, Bali alimfukuza mnyonge na mhitaji, Hata akamfisha mtu aliyevunjika moyo, 17 Naye alipenda kulaani, nako kukampata. Hakupendezwa na kubariki, kukawa mbali naye, 18 Alijivika laana kana kwamba ni vazi lake. Ikamwingilia moyoni kama maji, Na kama mafuta mifupani mwake. 19 Na iwe kwake kama vazi ajivikalo, Na kama mshipi ajifungao daima. 20 Ndiyo malipo ya washitaki wangu toka kwa Bwana, Na ya hao wanaoisingizia nafsi yangu mabaya. 21 Na Wewe, MUNGU, Bwana, unitendee kwa ajili ya jina lako, Kwa kuwa fadhili zako ni njema uniokoe. 22 Kwa maana mimi ni mnyonge na mhitaji, Na moyo wangu umejeruhi ndani yangu. 23 Ninapita kama kivuli kianzacho kutoweka, Ninapeperushwa kama nzige. 24 Magoti yangu yamedhoofu kwa kufunga, Na mwili wangu umekonda kwa kukosa mafuta. 25 Nami nalikuwa laumu kwao, Wanionapo hutikisa vichwa vyao. 26 Ee Bwana, Mungu wangu, unisaidie, Uniokoe sawasawa na fadhili zako. 27 Nao wakajue ya kuwa ndio mkono wako; Wewe, Bwana, umeyafanya hayo. 28 Wao walaani, bali Wewe utabariki, Wameondoka wao wakaaibishwa, Bali mtumishi wako atafurahi. 29 Washitaki wangu watavikwa fedheha, Watajivika aibu yao kama joho. 30 Nitamshukuru Bwana kwa kinywa changu, Naam, nitamsifu katikati ya mkutano. 31 Maana atasimama mkono wa kuume wa mhitaji Amwokoe na wanaoihukumu nafsi yake.

Zaburi 110

1 Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako. 2 Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; 3 Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. 4 Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki. 5 Bwana yu mkono wako wa kuume; Ataseta wafalme, Siku ya ghadhabu yake. 6 Atahukumu kati ya mataifa, Ataijaza nchi mizoga; Ataseta kichwa katika nchi nyingi. 7 Atakunywa maji ya mto njiani; Kwa hiyo atakiinua kichwa chake.

Zaburi 111

1 Haleluya Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote,Barazani pa wanyofu wa moyo na katika mkutano. 2 Matendo ya Bwana ni makuu, Yafikiriwa sana na wapendezwao nayo. 3 Kazi yake ni heshima na adhama, Na haki yake yakaa milele. 4 Amefanya ukumbusho wa matendo yake ya ajabu; Bwana ni mwenye fadhili na rehema. 5 Amewapa wamchao chakula; Atalikumbuka agano lake milele. 6 Amewajulisha watu wake uwezo wa matendo yake, Kwa kuwapa urithi wa mataifa. 7 Matendo ya mikono yake ni kweli na hukumu, Maagizo yake yote ni amini, 8 Yamethibitika milele na milele, Yamefanywa katika kweli na adili. 9 Amewapelekea watu wake ukombozi, Ameamuru agano lake liwe la milele, Jina lake ni takatifu la kuogopwa. 10 Kumcha Bwana ndio mwanzo wa hekima, Wote wafanyao hayo wana akili njema, Sifa zake zakaa milele.

Zaburi 112

1 Haleluya. Heri mtu yule amchaye Bwana, Apendezwaye sana na maagizo yake. 2 Wazao wake watakuwa hodari duniani; Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa. 3 Nyumbani mwake mna utajiri na mali, Na haki yake yakaa milele. 4 Nuru huwazukia wenye adili gizani; Ana fadhili na huruma na haki. 5 Heri atendaye fadhili na kukopesha; Atengenezaye mambo yake kwa haki. 6 Kwa maana hataondoshwa kamwe; Mwenye haki atakumbukwa milele. 7 Hataogopa habari mbaya; Moyo wake u imara ukimtumaini Bwana. 8 Moyo wake umethibitika hataogopa, Hata awaone watesi wake wameshindwa. 9 Amekirimu, na kuwapa maskini, Haki yake yakaa milele, Pembe yake itatukuzwa kwa utukufu. 10 Asiye haki ataona na kusikitika, Atasaga meno yake na kuyeyuka, Tamaa ya wasio haki itapotea.

Zaburi 113

1 Haleluya. Enyi watumishi wa Bwana, sifuni, Lisifuni jina la Bwana. 2 Jina la Bwana lihimidiwe Tangu leo na hata milele. 3 Toka maawio ya jua hata machweo yake Jina la Bwana husifiwa. 4 Bwana ni mkuu juu ya mataifa yote, Na utukufu wake ni juu ya mbingu. 5 Ni nani aliye mfano wa Bwana, Mungu wetu aketiye juu; 6 Anyenyekeaye kutazama, Mbinguni na duniani? 7 Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Na kumpandisha maskini kutoka jaani. 8 Amketishe pamoja na wakuu, Pamoja na wakuu wa watu wake. 9 Huweka nyumbani mwanamke aliye tasa, Awe mama ya watoto mwenye furaha.

Zaburi 114

1 Haleluya. Israeli alipotoka Misri, Na Yakobo katika watu wa lugha ya kigeni. 2 Yuda ilikuwa patakatifu pake, Israeli milki yake. 3 Bahari iliona ikakimbia, Yordani ilirudishwa nyuma. 4 Milima iliruka kama kondoo waume, Vilima kama wana-kondoo. 5 Ee bahari, una nini, ukimbie? Yordani, urudi nyuma? 6 Enyi milima, mruke kama kondoo waume? Enyi vilima, kama wana-kondoo? 7 Tetemeka, Ee nchi, mbele za uso wa Bwana, Mbele za uso wa Mungu wa Yakobo. 8 Augeuza mwamba kuwa ziwa la maji, Jiwe gumu kuwa chemchemi.

Zaburi 115

1 Ee Bwana, kutukuza usitutukuze sisi, Bali ulitukuze jina lako, Kwa ajili ya fadhili zako, Kwa ajili ya uaminifu wako. 2 Kwa nini mataifa kusema, Yuko wapi Mungu wao? 3 Lakini Mungu wetu yuko mbinguni, Alitakalo lote amelitenda. 4 Sanamu zao ni fedha na dhahabu, Kazi ya mikono ya wanadamu. 5 Zina vinywa lakini hazisemi, Zina macho lakini hazioni, 6 Zina masikio lakini hazisikii, Zina pua lakini hazisikii harufu, 7 Mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi, Wala hazitoi sauti kwa koo zake. 8 Wazifanyao watafanana nazo, Kila mmoja anayezitumainia. 9 Enyi Israeli, mtumainini Bwana; Yeye ni msaada wao na ngao yao. 10 Enyi mlango wa Haruni, mtumainini Bwana; Yeye ni msaada wao na ngao yao. 11 Enyi mmchao Bwana, mtumainini Bwana; Yeye ni msaada wao na ngao yao. 12 Bwana ametukumbuka, Naye atatubariki sisi. Ataubariki mlango wa Israeli, Ataubariki mlango wa Haruni, 13 Atawabariki wamchao Bwana, Wadogo kwa wakubwa. 14 Bwana na awaongeze ninyi, Ninyi na watoto wenu. 15 Na mbarikiwe ninyi na Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi. 16 Mbingu ni mbingu za Bwana, Bali nchi amewapa wanadamu. 17 Sio wafu wamsifuo Bwana, Wala wo wote washukao kwenye kimya; 18 Bali sisi tutamhimidi Bwana, Tangu leo na hata milele.

Zaburi 116

1 Haleluya. Nampenda Bwana kwa kuwa anaisikiliza Sauti yangu na dua zangu. 2 Kwa maana amenitegea sikio lake, Kwa hiyo nitamwita siku zangu zote. 3 Kamba za mauti zilinizunguka, Shida za kuzimu zilinipata. Naliona taabu na huzuni; 4 Nikaliitia jina la Bwana. Ee Bwana, nakuomba sana, Uniokoe nafsi yangu. 5 Bwana ni mwenye neema na haki, Naam, Mungu wetu ni mwenye rehema. 6 Bwana huwalinda wasio na hila; Nalidhilika, akaniokoa. 7 Ee nafsi yangu, urudi rahani mwako, Kwa kuwa Bwana amekutendea ukarimu. 8 Maana umeniponya nafsi yangu na mauti, Macho yangu na machozi, Na miguu yangu na kuanguka. 9 Nitaenenda mbele za Bwana Katika nchi za walio hai. 10 Naliamini, kwa maana nitasema, Mimi naliteswa sana. 11 Mimi nalisema kwa haraka yangu, Wanadamu wote ni waongo. 12 Nimrudishie Bwana nini Kwa ukarimu wake wote alionitendea? 13 Nitakipokea kikombe cha wokovu; Na kulitangaza jina la Bwana; 14 Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana, Naam, mbele ya watu wake wote. 15 Ina thamani machoni pa Bwana Mauti ya wacha Mungu wake. 16 Ee Bwana, hakika mimi ni mtumishi wako, Mtumishi wako, mwana wa mjakazi wako, Umevifungua vifungo vyangu. 17 Nitakutolea dhabihu ya kushukuru; Na kulitangaza jina la Bwana; 18 Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana, Naam, mbele ya watu wake wote. 19 Katika nyua za nyumba ya Bwana, Ndani yako, Ee Yerusalemu.

Zaburi 117

1 Haleluya. Enyi mataifa yote, msifuni Bwana, Enyi watu wote, mhimidini. 2 Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu, Na uaminifu wa Bwana ni wa milele.

Zaburi 118

1 Haleluya. Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele. 2 Israeli na aseme sasa, Ya kwamba fadhili zake ni za milele. 3 Mlango wa Haruni na waseme sasa, Ya kwamba fadhili zake ni za milele. 4 Wamchao Bwana na waseme sasa, Ya kwamba fadhili zake ni za milele. 5 Katika shida yangu nalimwita Bwana; Bwana akanijibu akaniweka panapo nafasi. 6 Bwana yuko upande wangu, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? 7 Bwana yuko upande wangu, msaidizi wangu, Kwa hiyo nitawaona wanaonichukia wameshindwa. 8 Ni heri kumkimbilia Bwana Kuliko kuwatumainia wanadamu. 9 Ni heri kumkimbilia Bwana. Kuliko kuwatumainia wakuu. 10 Mataifa yote walinizunguka; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. 11 Walinizunguka, naam, walinizunguka; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. 12 Walinizunguka kama nyuki, Walizimika kama moto wa miibani; Kwa jina la Bwana naliwakatilia mbali. 13 Ulinisukuma sana ili nianguke; Lakini Bwana akanisaidia. 14 Bwana ni nguvu zangu na wimbo wangu, Naye amekuwa wokovu wangu. 15 Sauti ya furaha na wokovu Imo hemani mwao wenye haki; Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu. 16 Mkono wa kuume wa Bwana umetukuzwa; Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu. 17 Sitakufa bali nitaishi, Nami nitayasimulia matendo ya Bwana. 18 Bwana ameniadhibu sana, Lakini hakuniacha nife. 19 Nifungulieni malango ya haki, Nitaingia na kumshukuru Bwana. 20 Lango hili ni la Bwana, Wenye haki ndio watakaoliingia. 21 Nitakushukuru kwa maana umenijibu, Nawe umekuwa wokovu wangu. 22 Jiwe walilolikataa waashi Limekuwa jiwe kuu la pembeni. 23 Neno hili limetoka kwa Bwana, Nalo ni ajabu machoni petu. 24 Siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana, Tutashangilia na kuifurahia. 25 Ee Bwana, utuokoe, twakusihi; Ee Bwana, utufanikishe, twakusihi. 26 Na abarikiwe yeye ajaye kwa jina la Bwana; Tumewabarikia toka nyumbani mwa Bwana. 27 Bwana ndiye aliye Mungu, Naye ndiye aliyetupa nuru. Ifungeni dhabihu kwa kamba Pembeni mwa madhabahu. 28 Ndiwe Mungu wangu, nami nitakushukuru, Ndiwe Mungu wangu, nami nitakutukuza. 29 Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele.

Zaburi 119

1 Heri walio kamili njia zao, Waendao katika sheria ya Bwana. 2 Heri wazitiio shuhuda zake, Wamtafutao kwa moyo wote. 3 Naam, hawakutenda ubatili, Wamekwenda katika njia zake. 4 Wewe umetuamuru mausia yako, Ili sisi tuyatii sana. 5 Ningependa njia zangu ziwe thabiti, Nizitii amri zako. 6 Ndipo mimi sitaaibika, Nikiyaangalia maagizo yako yote. 7 Nitakushukuru kwa unyofu wa moyo, Nikiisha kujifunza hukumu za haki yako 8 Nitazitii amri zako, Usiniache kabisa 9 Jinsi gani kijana aisafishe njia yake? Kwa kutii, akilifuata neno lako. 10 Kwa moyo wangu wote nimekutafuta, Usiniache nipotee mbali na maagizo yako. 11 Moyoni mwangu nimeliweka neno lako, Nisije nikakutenda dhambi. 12 Ee Bwana, umehimidiwa, Unifundishe amri zako. 13 Kwa midomo yangu nimezisimulia Hukumu zote za kinywa chako. 14 Nimeifurahia njia ya shuhuda zako Kana kwamba ni mali mengi. 15 Nitayatafakari mausia yako, Nami nitaziangalia njia zako. 16 Nitajifurahisha sana kwa amri zako, Sitalisahau neno lako. 17 Umtendee mtumishi wako ukarimu, Nipate kuishi, nami nitalitii neno lako. 18 Unifumbue macho yangu niyatazame Maajabu yatokayo katika sheria yako. 19 Mimi ni mgeni katika nchi, Usinifiche maagizo yako. 20 Roho yangu imepondeka kwa kutamani Hukumu zako kila wakati. 21 Umewakemea wenye kiburi, Wamelaaniwa waendao mbali na maagizo yako. 22 Uniondolee laumu na dharau, Kwa maana nimezishika shuhuda zako. 23 Wakuu nao waliketi wakaninena, Lakini mtumishi wako atazitafakari amri zako. 24 Shuhuda zako nazo ndizo furaha yangu, Na washauri wangu. 25 Nafsi yangu imeambatana na mavumbi, Unihuishe sawasawa na neno lako. 26 Nalizisimulia njia zangu ukanijibu, Unifundishe amri zako. 27 Unifahamishe njia ya mausia yako, Nami nitayatafakari maajabu yako. 28 Nafsi yangu imeyeyuka kwa uzito, Unitie nguvu sawasawa na neno lako. 29 Uniondolee njia ya uongo, Unineemeshe kwa sheria yako. 30 Nimeichagua njia ya uaminifu, Na kuziweka hukumu zako mbele yangu. 31 Nimeambatana na shuhuda zako, Ee Bwana, usiniaibishe. 32 Nitakwenda mbio katika njia ya maagizo yako, Utakaponikunjua moyo wangu. 33 Ee Bwana, unifundishe njia ya amri zako, Nami nitaishika hata mwisho. 34 Unifahamishe nami nitaishika sheria yako, Naam, nitaitii kwa moyo wangu wote. 35 Uniendeshe katika mapito ya maagizo yako, Kwa maana nimependezwa nayo. 36 Unielekeze moyo wangu na shuhuda zako, Wala usiielekee tamaa. 37 Unigeuze macho yangu nisitazame visivyofaa, Unihuishe katika njia yako. 38 Umthibitishie mtumishi wako ahadi yako, Inayohusu kicho chako. 39 Uniondolee laumu niiogopayo, Maana hukumu zako ni njema. 40 Tazama, nimeyatamani mausia yako, Unihuishe kwa haki yako. 41 Ee Bwana, fadhili zako zinifikie na mimi, Naam, wokovu wako sawasawa na ahadi yako. 42 Nami nitamjibu neno anilaumuye, Kwa maana nalitumainia neno lako. 43 Usiliondoe neno la kweli kinywani mwangu kamwe, Maana nimezingojea hukumu zako. 44 Nami nitaitii sheria yako daima, Naam, milele na milele. 45 Nami nitakwenda panapo nafasi, Kwa kuwa nimejifunza mausia yako. 46 Nitazinena shuhuda zako mbele ya wafalme, Wala sitaona aibu. 47 Nami nitajifurahisha sana kwa maagizo yako, Ambayo nimeyapenda. 48 Na mikono yangu nitayainulia maagizo yako niliyoyapenda, Nami nitazitafakari amri zako. 49 Likumbuke neno ulilomwambia mtumishi wako, Kwa sababu umenitumainisha. 50 Hii ndiyo faraja yangu katika taabu yangu, Ya kwamba ahadi yako imenihuisha. 51 Wenye kiburi wamenidharau mno, Sikujiepusha na sheria zako. 52 Nimezikumbuka hukumu zako za kale, Ee Bwana, nikajifariji. 53 Ghadhabu imenishika kwa sababu ya wasio haki, Waiachao sheria yako. 54 Amri zako zimekuwa nyimbo zangu, Katika nyumba ya ugeni wangu. 55 Wakati wa usiku nimelikumbuka jina lako, Ee Bwana, nikaitii sheria yako. 56 Hayo ndiyo niliyokuwa nayo, Kwa sababu nimeyashika mausia yako. 57 Bwana ndiye aliye fungu langu, Nimesema kwamba nitayatii maneno yake. 58 Nimekuomba radhi kwa moyo wangu wote, Unifadhili sawasawa na ahadi yako. 59 Nalizitafakari njia zangu, Na miguu yangu nalizielekezea shuhuda zako. 60 Nalifanya haraka wala sikukawia, Kuyatii maagizo yako. 61 Kamba za wasio haki zimenifunga, Sikuisahau sheria yako. 62 Katikati ya usiku nitaamka nikushukuru, Kwa sababu ya hukumu zako za haki. 63 Mimi ni mwenzao watu wote wakuchao, Na wale wayatiio mausia yako. 64 Bwana, dunia imejaa fadhili zako, Unifundishe amri zako. 65 Umemtendea mema mtumishi wako, Ee Bwana, sawasawa na neno lako. 66 Unifundishe akili na maarifa, Maana nimeyaamini maagizo yako. 67 Kabla sijateswa mimi nalipotea, Lakini sasa nimelitii neno lako. 68 Wewe U mwema na mtenda mema, Unifundishe amri zako. 69 Wenye kiburi wamenizulia uongo, Kwa moyo wangu wote nitayashika mausia yako. 70 Mioyo yao imenenepa kama shahamu, Mimi nimeifurahia sheria yako. 71 Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, Nipate kujifunza amri zako. 72 Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu, Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha. 73 Mikono yako ilinifanya ikanitengeneza, Unifahamishe nikajifunze maagizo yako. 74 Wakuchao na wanione na kufurahi, Kwa sababu nimelingojea neno lako. 75 Najua ya kuwa hukumu zako ni za haki, Ee Bwana, na kwa uaminifu umenitesa. 76 Nakuomba, fadhili zako ziwe faraja kwangu, Sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako. 77 Rehema zako zinijie nipate kuishi, Maana sheria yako ni furaha yangu. 78 Wenye kiburi waaibike, maana wamenidhulumu kwa uongo, Mimi nitayatafakari mausia yako. 79 Wakuchao na wanirudie, Nao watazijua shuhuda zako. 80 Moyo wangu na uwe mkamilifu katika amri zako, Nisije mimi nikaaibika. 81 Nafsi yangu imefifia kwa kuutamani wokovu wako, Nimelingojea neno lako. 82 Macho yangu yamefifia kwa kuitazamia ahadi yako, Nisemapo, Lini utakaponifariji? 83 Maana nimekuwa kama kiriba katika moshi, Sikuzisahau amri zako. 84 Siku za mtumishi wako ni ngapi, Lini utakapowahukumu wale wanaonifuatia? 85 Wenye kiburi wamenichimbia mashimo, Ambao hawaifuati sheria yako. 86 Maagizo yako yote ni amini, Wananifuatia bure, unisaidie. 87 Walikuwa karibu na kunikomesha katika nchi, Lakini sikuyaacha mausia yako. 88 Unihuishe kwa fadhili zako, Nami nitazishika shuhuda za kinywa chako. 89 Ee Bwana, neno lako lasimama Imara mbinguni hata milele. 90 Uaminifu wako upo kizazi baada ya kizazi, Umeiweka nchi, nayo inakaa. 91 Kwa hukumu zako vimesimama imara hata leo, Maana vitu vyote ni watumishi wako. 92 Kama sheria yako isingalikuwa furaha yangu, Hapo ningalipotea katika taabu zangu. 93 Hata milele sitayasahau maagizo yako, Maana kwa hayo umenihuisha. 94 Mimi ni wako, uniokoe, Kwa maana nimejifunza mausia yako. 95 Wasio haki wameniotea ili kunipoteza, Nitazitafakari shuhuda zako. 96 Nimeona ukamilifu wote kuwa na mwisho, Bali agizo lako ni pana mno. 97 Sheria yako naipenda mno ajabu, Ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa. 98 Maagizo yako hunitia hekima kuliko adui zangu, Kwa maana ninayo sikuzote. 99 Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote, Maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo. 100 Ninao ufahamu kuliko wazee, Kwa kuwa nimeyashika mausia yako. 101 Nimeiepusha miguu yangu na kila njia mbaya, Ili nilitii neno lako. 102 Sikujiepusha na hukumu zako, Maana Wewe mwenyewe umenifundisha. 103 Mausia yako ni matamu sana kwangu, Kupita asali kinywani mwangu. 104 Kwa mausia yako najipatia ufahamu, Ndiyo maana naichukia kila njia ya uongo. 105 Neno lako ni taa ya miguu yangu, Na mwanga wa njia yangu. 106 Nimeapa nami nitaifikiliza, Kuzishika hukumu za haki yako. 107 Nimeteswa mno; Ee Bwana, unihuishe sawasawa na neno lako. 108 Ee Bwana, uziridhie sadaka za kinywa changu, Na kunifundisha hukumu zako. 109 Nafsi yangu imo mkononi mwangu daima, Lakini sheria yako sikuisahau. 110 Watendao uovu wamenitegea mtego, Lakini sikuikosa njia ya mausia yako. 111 Shuhuda zako nimezifanya urithi wa milele, Maana ndizo changamko la moyo wangu. 112 Nimeuelekeza moyo wangu nizitende amri zako, Daima, naam, hata milele. 113 Watu wa kusita-sita nawachukia, Lakini sheria yako naipenda. 114 Ndiwe sitara yangu na ngao yangu, Neno lako nimelingojea. 115 Enyi watenda mabaya, ondokeni kwangu, Niyashike maagizo ya Mungu wangu. 116 Unitegemeze sawasawa na ahadi yako, nikaishi, Wala usiniache niyaaibikie matumaini yangu. 117 Unisaidie nami nitakuwa salama, Nami nitaziangalia amri zako daima. 118 Umewakataa wote wazikosao amri zako, Kwa maana hila zao ni uongo. 119 Wabaya wa nchi pia umewaondoa kama takataka, Ndiyo maana nimezipenda shuhuda zako. 120 Mwili wangu unatetemeka kwa kukucha Wewe, Nami ninaziogopa hukumu zako. 121 Nimefanya hukumu na haki, Usiniache mikononi mwao wanaonionea. 122 Uwe mdhamini wa mtumishi wako, apate mema, Wenye kiburi wasinionee. 123 Macho yangu yamefifia kwa kuutamani wokovu wako, Na ahadi ya haki yako. 124 Kama zilivyo rehema zako umtendee mtumishi wako, Na amri zako unifundishe. 125 Mimi ni mtumishi wako, unifahamishe, Nipate kuzijua shuhuda zako. 126 Wakati umewadia Bwana atende kazi; Kwa kuwa wameitangua sheria yako. 127 Ndiyo maana nimeyapenda maagizo yako, Kuliko dhahabu, naam, dhahabu iliyo safi. 128 Maana nayaona mausia yako yote kuwa ya adili, Kila njia ya uongo naichukia. 129 Shuhuda zako ni za ajabu, Ndiyo maana roho yangu imezishika. 130 Kufafanusha maneno yako kwatia nuru, Na kumfahamisha mjinga. 131 Nalifunua kinywa changu nikatweta, Maana naliyatamani maagizo yako. 132 Unigeukie, unirehemu mimi, Kama iwahusuvyo walipendao jina lako. 133 Uzielekeze hatua zangu kwa neno lako, Uovu usije ukanimiliki. 134 Unikomboe na dhuluma ya mwanadamu, Nipate kuyashika mausia yako. 135 Umwangazie mtumishi wako uso wako, Na kunifundisha amri zako. 136 Macho yangu yachuruzika mito ya maji, Kwa sababu hawaitii sheria yako. 137 Ee Bwana, Wewe ndiwe mwenye haki, Na hukumu zako ni za adili. 138 Umeziagiza shuhuda zako kwa haki, Na kwa uaminifu mwingi. 139 Juhudi yangu imeniangamiza, Maana watesi wangu wameyasahau maneno yako. 140 Neno lako limesafika sana, Kwa hiyo mtumishi wako amelipenda. 141 Mimi ni mdogo, nadharauliwa, Lakini siyasahau mausia yako. 142 Haki yako ni haki ya milele, Na sheria yako ni kweli. 143 Taabu na dhiki zimenipata, Maagizo yako ni furaha yangu. 144 Haki ya shuhuda zako ni ya milele, Unifahamishe, nami nitaishi. 145 Nimeita kwa moyo wangu wote; Ee Bwana, uitike; Nitazishika amri zako. 146 Nimekuita Wewe, uniokoe, Nami nitazishika shuhuda zako. 147 Kutangulia mapambazuko naliomba msaada, Naliyangojea maneno yako kwa tumaini. 148 Macho yangu yalitangulia makesha ya usiku, Ili kuitafakari ahadi yako. 149 Uisikie sauti yangu sawasawa na fadhili zako, Ee Bwana, unihuishe sawasawa na hukumu yako. 150 Wanakaribia wanaonifuatia kwa chuki, Wamekwenda mbali na sheria yako. 151 Ee Bwana, Wewe U karibu, Na maagizo yako yote ni kweli. 152 Tokea zamani nimejua kwa shuhuda zako, Ya kuwa umeziweka zikae milele. 153 Uyaangalie mateso yangu, uniokoe, Maana sikuisahau sheria yako. 154 Unitetee na kunikomboa, Unihuishe sawasawa na ahadi yako. 155 Wokovu u mbali na wasio haki, Kwa maana hawajifunzi amri zako. 156 Ee Bwana, rehema zako ni nyingi, Unihuishe sawasawa na hukumu zako. 157 Wanaonifuatia na watesi wangu ni wengi, Lakini sikujiepusha na shuhuda zako. 158 Nimewaona watendao uhaini nikachukizwa, Kwa sababu hawakulitii neno lako. 159 Uangalie niyapendavyo mausia yako, Ee Bwana, unihuishe sawasawa na fadhili zako. 160 Jumla ya neno lako ni kweli, Na kila hukumu ya haki yako ni ya milele. 161 Wakuu wameniudhi bure, Ila moyo wangu unayahofia maneno yako. 162 Naifurahia ahadi yako, Kama apataye mateka mengi. 163 Nimeuchukia uongo, umenikirihi, Sheria yako nimeipenda. 164 Mara saba kila siku nakusifu, Kwa sababu ya hukumu za haki yako. 165 Wana amani nyingi waipendao sheria yako, Wala hawana la kuwakwaza. 166 Ee Bwana, nimeungojea wokovu wako, Na maagizo yako nimeyatenda. 167 Nafsi yangu imezishika shuhuda zako, Nami nazipenda mno. 168 Nimeyashika mausia yako na shuhuda zako, Maana njia zangu zote zi mbele zako. 169 Ee Bwana, kilio changu na kikukaribie, Unifahamishe sawasawa na neno lako. 170 Dua yangu na ifike mbele zako, Uniponye sawasawa na ahadi yako. 171 Midomo yangu na itoe sifa, Kwa kuwa unanifundisha mausia yako. 172 Ulimi wangu na uiimbe ahadi yako, Maana maagizo yako yote ni ya haki. 173 Mkono wako na uwe tayari kunisaidia, Maana nimeyachagua mausia yako. 174 Ee Bwana, nimeutamani wokovu wako, Na sheria yako ndiyo furaha yangu. 175 Nafsi yangu na iishi, ipate kukusifu, Na hukumu zako zinisaidie. 176 Nimetanga-tanga kama kondoo aliyepotea; Umtafute mtumishi wako; Kwa maana sikuyasahau maagizo yako.

Zaburi 120

1 Katika shida yangu nalimlilia Bwana Naye akaniitikia. 2 Ee Bwana, uiponye nafsi yangu Na midomo ya uongo na ulimi wa hila. 3 Akupe nini, akuzidishie nini, Ewe ulimi wenye hila? 4 Mishale ya mtu hodari iliyochongoka, Pamoja na makaa ya mretemu. 5 Ole wangu mimi! Kwa kuwa nimekaa katika Mesheki; Na kufanya maskani yangu Katikati ya hema za Kedari. 6 Nafsi yangu imekaa siku nyingi, Pamoja naye aichukiaye amani. 7 Mimi ni wa amani; Bali ninenapo, wao huelekea vita.

Zaburi 121

1 Nitayainua macho yangu niitazame milima, Msaada wangu utatoka wapi? 2 Msaada wangu u katika Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi. 3 Asiuache mguu wako usogezwe; Asisinzie akulindaye; 4 Naam, hatasinzia wala hatalala usingizi, Yeye aliye mlinzi wa Israeli. 5 Bwana ndiye mlinzi wako; Bwana ni uvuli mkono wako wa kuume. 6 Jua halitakupiga mchana, Wala mwezi wakati wa usiku. 7 Bwana atakulinda na mabaya yote, Atakulinda nafsi yako. 8 Bwana atakulinda utokapo na uingiapo, Tangu sasa na hata milele.

Zaburi 122

1 Nalifurahi waliponiambia, Na twende nyumbani kwa Bwana. 2 Miguu yetu imesimama Ndani ya malango yako, Ee Yerusalemu. 3 Ee Yerusalemu uliyejengwa Kama mji ulioshikamana, 4 Huko ndiko walikopanda kabila, Kabila za Bwana; Ushuhuda kwa Israeli, Walishukuru jina la Bwana. 5 Maana huko viliwekwa viti vya hukumu, Viti vya enzi vya mbari ya Daudi. 6 Utakieni Yerusalemu amani; Na wafanikiwe wakupendao; 7 Amani na ikae ndani ya kuta zako, Na kufanikiwa ndani ya majumba yako. 8 Kwa ajili ya ndugu zangu na rafiki zangu Niseme sasa, Amani ikae nawe. 9 Kwa ajili ya nyumba ya Bwana, Mungu wetu, Nikutafutie mema.

Zaburi 123

1 Nimekuinulia macho yangu, Wewe uketiye mbinguni. 2 Kama vile macho ya watumishi Kwa mkono wa bwana zao Kama macho ya mjakazi Kwa mkono wa bibi yake; Hivyo macho yetu humwelekea Bwana, Mungu wetu, Hata atakapoturehemu. 3 Uturehemu, Ee Bwana, uturehemu sisi, Kwa maana tumeshiba dharau. 4 Nafsi zetu zimeshiba mzaha wa wenye raha, Na dharau ya wenye kiburi.

Zaburi 124

1 Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa, 2 Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Wanadamu walipotushambulia. 3 Papo hapo wangalitumeza hai, Hasira yao ilipowaka juu yetu 4 Papo hapo maji yangalitugharikisha, Mto ungalipita juu ya roho zetu; 5 Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu Maji yafurikayo. 6 Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. 7 Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. 8 Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.

Zaburi 125

1 Wamtumainio Bwana ni kama mlima Sayuni, Ambao hautatikisika, wakaa milele. 2 Kama milima inavyouzunguka Yerusalemu, Ndivyo Bwana anavyowazunguka watu wake, Tangu sasa na hata milele. 3 Kwa maana fimbo ya udhalimu Haitakaa juu ya fungu la wenye haki; Wenye haki wasije wakainyosha Mikono yao kwenye upotovu. 4 Ee Bwana, uwatendee mema walio wema, Nao walio wanyofu wa moyo. 5 Bali wao wanaozigeukia njia zao zilizopotoka, Bwana atawaondoa pamoja na watenda maovu. Amani ikae na Israeli.

Zaburi 126

1 Bwana alipowarejeza mateka wa Sayuni, Tulikuwa kama waotao ndoto. 2 Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko, Na ulimi wetu kelele za furaha. Ndipo waliposema katika mataifa, Bwana amewatendea mambo makuu. 3 Bwana alitutendea mambo makuu, Tulikuwa tukifurahi. 4 Ee Bwana, uwarejeze watu wetu waliofungwa, Kama vijito vya Kusini. 5 Wapandao kwa machozi Watavuna kwa kelele za furaha. 6 Ingawa mtu anakwenda zake akilia, Azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, Aichukuapo miganda yake.

Zaburi 127

1 Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure. 2 Kazi yenu ni bure, mnaoamka mapema, Na kukawia kwenda kulala, Na kula chakula cha taabu; Yeye humpa mpenzi wake usingizi. 3 Tazama, wana ndio urithi wa Bwana, Uzao wa tumbo ni thawabu. 4 Kama mishale mkononi mwa shujaa, Ndivyo walivyo wana wa ujanani. 5 Heri mtu yule Aliyelijaza podo lake hivyo. Naam, hawataona aibu Wanaposema na adui langoni.

Zaburi 128

1 Heri kila mtu amchaye Bwana, Aendaye katika njia yake. 2 Taabu ya mikono yako hakika utaila; Utakuwa heri, na kwako kwema. 3 Mkeo atakuwa kama mzabibu uzaao, Vyumbani mwa nyumba yako. Wanao kama miche ya mizeituni Wakiizunguka meza yako. 4 Tazama, atabarikiwa hivyo, yule amchaye Bwana. 5 Bwana akubariki toka Sayuni; Uone uheri wa Yerusalemu siku zote za maisha yako; 6 Naam, ukawaone wana wa wanao. Amani ikae na Israeli.

Zaburi 129

1 Mara nyingi wamenitesa tangu ujana wangu, Israeli na aseme sasa, 2 Mara nyingi wamenitesa tangu ujana wangu, Lakini hawakuniweza. 3 Wakulima wamelima mgongoni mwangu, Wamefanya mirefu mifuo yao. 4 Bwana ndiye mwenye haki, Amezikata kamba zao wasio haki. 5 Na waaibishwe, warudishwe nyuma, Wote wanaoichukia Sayuni. 6 Na wawe kama majani ya darini Yanyaukayo kabla hayajamea. 7 Ambayo mvunaji haujazi mkono wake, Wala mfunga miganda kifua chake. 8 Wala hawasemi wapitao, Amani ya Bwana ikae nanyi, Twawabariki kwa jina la Bwana.

Zaburi 130

1 Ee Bwana, toka vilindini nimekulilia. 2 Bwana, uisikie sauti yangu. Masikio yako na yaisikilize Sauti ya dua zangu. 3 Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? 4 Lakini kwako kuna msamaha, Ili Wewe uogopwe. 5 Nimemngoja Bwana, roho yangu imengoja, Na neno lake nimelitumainia. 6 Nafsi yangu inamngoja Bwana, Kuliko walinzi waingojavyo asubuhi, Naam, walinzi waingojao asubuhi. 7 Ee Israeli, umtarajie Bwana; Maana kwa Bwana kuna fadhili, Na kwake kuna ukombozi mwingi. 8 Yeye atamkomboa Israeli na maovu yake yote.

Zaburi 131

1 Bwana, moyo wangu hauna kiburi, Wala macho yangu hayainuki. Wala sijishughulishi na mambo makuu, Wala na mambo yashindayo nguvu zangu. 2 Hakika nimeituliza nafsi yangu, Na kuinyamazisha. Kama mtoto aliyeachishwa Kifuani mwa mama yake; Kama mtoto aliyeachishwa, Ndivyo roho yangu ilivyo kwangu. 3 Ee Israeli, umtarajie Bwana, Tangu leo na hata milele.

Zaburi 132

1 Bwana, umkumbukie Daudi Taabu zake zote alizotaabika. 2 Ndiye aliyemwapia Bwana, Akaweka nadhiri kwa Shujaa wa Yakobo. 3 Sitaingia hemani mwa nyumba yangu, Wala sitapanda matandiko ya kitanda changu; 4 Sitaacha macho yangu kuwa na usingizi, Wala kope zangu kusinzia; 5 Hata nitakapompatia Bwana mahali, Na Shujaa wa Yakobo maskani. 6 Tazama, tulisikia habari zake katika Efrata, Katika konde la Yearimu tuliiona. 7 Na tuingie katika maskani yake, Tusujudu penye kiti cha kuwekea miguu yake. 8 Ee Bwana, uinuke, uende kwenye raha yako, Wewe na sanduku la nguvu zako. 9 Makuhani wako na wavikwe haki, Watauwa wako na washangilie. 10 Kwa ajili ya Daudi, mtumishi wako, Usiurudishe nyuma uso wa masihi 11 Bwana amemwapia Daudi neno la kweli, Hatarudi nyuma akalihalifu, Baadhi ya wazao wa mwili wako Nitawaweka katika kiti chako cha enzi. 12 Wanao wakiyashika maagano yangu, Na shuhuda nitakazowafundisha; Watoto wao nao wataketi Katika kiti chako cha enzi milele. 13 Kwa kuwa Bwana ameichagua Sayuni, Ameitamani akae ndani yake. 14 Hapo ndipo mahali pangu pa raha milele, Hapo nitakaa kwa maana nimepatamani. 15 Hakika nitavibariki vyakula vyake Wahitaji wake nitawashibisha chakula. 16 Na makuhani wake nitawavika wokovu, Na watauwa wake watashangilia. 17 Hapo nitamchipushia Daudi pembe, Na taa nimemtengenezea masihi wangu. 18 Adui zake nitawavika aibu, Bali juu yake taji yake itasitawi.

Zaburi 133

1 Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. 2 Ni kama mafuta mazuri kichwani, Yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, Yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. 3 Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko Bwana alikoamuru baraka, Naam, uzima hata milele.

Zaburi 134

1 Tazama, enyi watumishi wa Bwana, Mhimidini Bwana, nyote pia. Ninyi mnaosimama usiku Katika nyumba ya Bwana. 2 Painulieni patakatifu mikono yenu, Na kumhimidi Bwana. 3 Bwana akubariki toka Sayuni, Aliyezifanya mbingu na nchi.

Zaburi 135

1 Haleluya. Lisifuni jina la Bwana, Enyi watumishi wa Bwana, sifuni. 2 Ninyi msimamao nyumbani mwa Bwana, Nyuani mwa nyumba ya Mungu wenu. 3 Msifuni Bwana kwa kuwa Bwana ni mwema, Liimbieni jina lake kwa maana lapendeza. 4 Kwa sababu Bwana amejichagulia Yakobo, Na Israeli, wawe watu wake hasa. 5 Maana najua mimi ya kuwa Bwana ni mkuu, Na Bwana wetu yu juu ya miungu yote. 6 Bwana amefanya kila lililompendeza, Katika mbingu na katika nchi, Katika bahari na katika vilindi vyote. 7 Ndiye apandishaye mvuke toka miisho ya nchi; Huifanyia mvua umeme; Hutoa upepo katika hazina zake. 8 Aliwapiga wazaliwa wa kwanza wa Misri, Wa wanadamu na wa wanyama. 9 Alipeleka ishara na maajabu kati yako, Ee Misri, Juu ya Farao na watumishi wake wote. 10 Aliwapiga mataifa mengi, Akawaua wafalme wenye nguvu; 11 Sihoni, mfalme wa Waamori, Na Ogu, mfalme wa Bashani, Na falme zote za Kanaani. 12 Akaitoa nchi yao iwe urithi, Urithi wa Israeli watu wake. 13 Ee Bwana, jina lako ni la milele, Bwana, kumbukumbu lako vizazi hata vizazi. 14 Kwa kuwa Bwana atawaamua watu wake, Atawahurumia watumishi wake. 15 Sanamu za mataifa ni fedha na dhahabu, Kazi ya mikono ya wanadamu. 16 Zina vinywa lakini hazisemi, Zina macho lakini hazioni, 17 Zina masikio lakini hazisikii, Wala hamna pumzi vinywani mwake. 18 Wazifanyao watafanana nazo, Na kila mmoja anayezitumainia. 19 Enyi mlango wa Israeli, mhimidini Bwana; Enyi mlango wa Haruni, mhimidini Bwana; 20 Enyi mlango wa Lawi, mhimidini Bwana; Ninyi mnaomcha Bwana, mhimidini Bwana. 21 Na ahimidiwe Bwana toka Sayuni, Akaaye Yerusalemu. Haleluya.

Zaburi 136

1 Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 2 Mshukuruni Mungu wa miungu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 3 Mshukuruni Bwana wa mabwana; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 4 Yeye peke yake afanya maajabu makuu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 5 Yeye aliyefanya mbingu kwa fahamu zake; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 6 Yeye aliyeitandaza nchi juu ya maji; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 7 Yeye aliyefanya mianga mikubwa; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 8 Jua litawale mchana; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 9 Mwezi na nyota zitawale usiku; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 10 Yeye aliyewapiga Wamisri kwa kuwaua wazaliwa wa kwanza wao; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 11 Akawatoa Waisraeli katikati yao; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 12 Kwa mkono hodari na mkono ulionyoshwa; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 13 Yeye aliyeigawa Bahari ya Shamu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 14 Akawavusha Israeli katikati yake; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 15 Akamwangusha Farao na jeshi lake katika Bahari ya Shamu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 16 Yeye aliyewaongoza watu wake jangwani; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 17 Yeye aliyewapiga wafalme wakuu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 18 Akawaua wafalme mashuhuri; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 19 Sihoni, mfalme wa Waamori; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 20 Na Ogu, mfalme wa Bashani; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 21 Akaitoa nchi yao iwe urithi; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 22 Urithi wa Israeli mtumishi wake; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 23 Aliyetukumbuka katika unyonge wetu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 24 Akatuokoa na watesi wetu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 25 Kila chenye mwili akipa chakula chake; Kwa maana fadhili zake ni za milele. 26 Mshukuruni Mungu wa mbingu; Kwa maana fadhili zake ni za milele.

Zaburi 137

1 Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi, Tukalia tulipoikumbuka Sayuni. 2 Katika miti iliyo katikati yake Tulivitundika vinubi vyetu. 3 Maana huko waliotuchukua mateka Walitaka tuwaimbie; Na waliotuonea walitaka furaha; Tuimbieni baadhi ya nyimbo za Sayuni. 4 Tuuimbeje wimbo wa Bwana Katika nchi ya ugeni? 5 Ee Yerusalemu, nikikusahau wewe, Mkono wangu wa kuume na usahau. 6 Ulimi wangu na ugandamane Na kaakaa la kinywa changu, nisipokukumbuka. Nisipoikuza Yerusalemu Zaidi ya furaha yangu iliyo kuu. 7 Ee Bwana, uwakumbuke wana wa Edomu, Siku ya Yerusalemu. Waliosema, Bomoeni! Bomoeni hata misingini! 8 Ee binti Babeli, uliye karibu na kuangamia, Heri atakayekupatiliza, ulivyotupatiliza sisi. 9 Heri yeye atakayewakamata wadogo wako, Na kuwaseta wao juu ya mwamba.

Zaburi 138

1 Nitakushukuru kwa moyo wangu wote, Mbele ya miungu nitakuimbia zaburi. 2 Nitasujudu nikilikabili hekalu lako takatifu, Nitalishukuru jina lako, Kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako, Kwa maana umeikuza ahadi yako, Kuliko jina lako lote. 3 Siku ile niliyokuita uliniitikia, Ukanifariji nafsi kwa kunitia nguvu. 4 Ee Bwana, wafalme wote wa dunia watakushukuru, Watakapoyasikia maneno ya kinywa chako. 5 Naam, wataziimba njia za Bwana, Kwa maana utukufu wa Bwana ni mkuu. 6 Ingawa Bwana yuko juu, amwona mnyenyekevu, Naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali. 7 Nijapokwenda kati ya shida utanihuisha, Utanyosha mkono juu ya hasira ya adui zangu, Na mkono wako wa kuume utaniokoa. 8 Bwana atanitimilizia mambo yangu; Ee Bwana, fadhili zako ni za milele; Usiziache kazi za mikono yako.

Zaburi 139

1 Ee Bwana, umenichunguza na kunijua. 2 Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu; Umelifahamu wazo langu tokea mbali. 3 Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu, Umeelewa na njia zangu zote. 4 Maana hamna neno ulimini mwangu Usilolijua kabisa, Bwana. 5 Umenizingira nyuma na mbele, Ukaniwekea mkono wako. 6 Maarifa hayo ni ya ajabu, yanishinda mimi, Hayadirikiki, siwezi kuyafikia. 7 Niende wapi nijiepushe na roho yako? Niende wapi niukimbie uso wako? 8 Kama ningepanda mbinguni, Wewe uko; Ningefanya kuzimu kitanda changu, Wewe uko. 9 Ningezitwaa mbawa za asubuhi, Na kukaa pande za mwisho za bahari; 10 Huko nako mkono wako utaniongoza, Na mkono wako wa kuume utanishika. 11 Kama nikisema, Hakika giza litanifunika, Na nuru inizungukayo ingekuwa usiku; 12 Giza nalo halikufichi kitu, Bali usiku huangaza kama mchana; Giza na mwanga kwako ni sawasawa. 13 Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu, Uliniunga tumboni mwa mama yangu. 14 Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, Na nafsi yangu yajua sana, 15 Mifupa yangu haikusitirika kwako, Nilipoumbwa kwa siri, Nilipoungwa kwa ustadi pande za chini za nchi; 16 Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; Chuoni mwako ziliandikwa zote pia, Siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado. 17 Mungu, fikira zako zina thamani nyingi kwangu; Jinsi ilivyo kubwa jumla yake! 18 Kama ningezihesabu ni nyingi kuliko mchanga; Niamkapo nikali pamoja nawe. 19 Ee Mungu, laiti ungewafisha waovu! Enyi watu wa damu, ondokeni kwangu; 20 Kwa maana wakuasi kwa ubaya, Adui zako wakutaja jina lako bure. 21 Je! Bwana nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? 22 Nawachukia kwa ukomo wa chuki, Wamekuwa adui kwangu. 23 Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, Unijaribu, uyajue mawazo yangu; 24 Uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu, Ukaniongoze katika njia ya milele.

Zaburi 140

1 Ee Bwana, uniokoe na mtu mbaya, Unihifadhi na mtu wa jeuri. 2 Waliowaza mabaya mioyoni mwao, Kila siku huondokesha vita. 3 Wamenoa ndimi zao kama nyoka, Sumu ya fira i chini ya midomo yao. 4 Ee Bwana, unilinde na mikono ya mtu asiye haki; Unihifadhi na mtu wa jeuri; Waliowaza kuzipotosha hatua zangu. 5 Wenye kiburi wamenifichia mtego na kamba; Wametandika wavu kando ya njia; Wameniwekea matanzi. 6 Nimemwambia Bwana, Ndiwe Mungu wangu; Ee Bwana, uisikie sauti ya dua zangu. 7 Ee MUNGU Bwana, nguvu za wokovu wangu, Umenifunika kichwa changu siku ya vita. 8 Ee Bwana, usimpe asiye haki tamaa zake, Usiifanikishe hila yake, wasije wakajiinua. 9 Nao wainuapo vichwa watu wanaonizunguka, Madhara ya midomo yao yawafunike. 10 Makaa ya moto yawaangukie, watupwe motoni, Na katika mashimo, wasipate kusimama tena. 11 Msingiziaji hatawekwa imara katika nchi, Mtu wa jeuri, uovu humwinda kumwangamiza. 12 Najua ya kuwa Bwana atamfanyia mnyonge hukumu, Na wahitaji haki yao. 13 Hakika wenye haki watalishukuru jina lako, Wenye adili watakaa mahali ulipo Wewe.

Zaburi 141

1 Ee Bwana, nimekuita, unijie hima, Uisikie sauti yangu nikuitapo. 2 Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba, Kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni. 3 Ee Bwana, uweke mlinzi kinywani pangu, Mngojezi mlangoni pa midomo yangu. 4 Usiuelekeze moyo wangu kunako jambo baya, Nisiyazoelee matendo yasiyofaa, Pamoja na watu watendao maovu; Wala nisile vyakula vyao vya anasa. 5 Mwenye haki na anipige, itakuwa fadhili; Anikemee, itakuwa kama mafuta kichwani; Kichwa changu kisikatae, Maana siachi kusali kati ya mabaya yao. 6 Makadhi wao wakiangushwa kando ya genge, Watayasikia maneno yangu, maana ni matamu. 7 Kama kupasua kuni na kuzichanja juu ya nchi, Ndivyo ilivyo mifupa yetu mdomoni pa kuzimu. 8 Macho yangu yanakuelekea Wewe, MUNGU Bwana, Nimekukimbilia Wewe, usiniache nafsi yangu. 9 Unilinde na mtego walionitegea, Na matanzi yao watendao maovu. 10 Wabaya na waanguke katika nyavu zao wenyewe, Pindi mimi ninapopita salama.

Zaburi 142

1 Kwa sauti yangu nitamlilia Bwana, Kwa sauti yangu nitamwomba Bwana dua. 2 Nitafunua mbele zake malalamiko yangu, Shida yangu nitaitangaza mbele zake. 3 Nilipozimia roho uliyajua mapito yangu; Katika njia niendayo wamenifichia mtego. 4 Utazame mkono wa kuume ukaone, Kwa maana sina mtu anijuaye. Makimbilio yamenipotea, Hakuna wa kunitunza roho. 5 Bwana, nimekuita nikasema, Ndiwe kimbilio langu, Fungu langu katika nchi ya walio hai. 6 Ukisikilize kilio changu, Kwa maana nimedhilika sana. Uniponye nao wanaonifuatia, Kwa maana wao ni hodari kuliko mimi. 7 Uitoe nafsi yangu kifungoni. Nipate kulishukuru jina lako. Wenye haki watanizunguka, Kwa kuwa Wewe unanikirimu.

Zaburi 143

1 Ee Bwana, uisikie sala yangu, uzisikilize dua zangu, Kwa uaminifu wako unijibu kwa haki yako. 2 Wala usimhukumu mtumishi wako, Maana kwako hakuna aliye hai mwenye haki. 3 Maana adui ameifuatia nafsi yangu, Ameutupa chini uzima wangu. Amenikalisha mahali penye giza, Kama watu waliokufa zamani. 4 Na roho yangu imezimia ndani yangu, Moyo wangu ndani yangu umesituka. 5 Nimezikumbuka siku za kale, Nimeyatafakari matendo yako yote, Naziwaza kazi za mikono yako. 6 Nakunyoshea mikono yangu; Nafsi yangu inakuonea kiu kama nchi kame. 7 Ee Bwana, unijibu hima, roho yangu imelegea; Usinifiche uso wako, Nisifanane nao washukao shimoni 8 Unifanye kusikia fadhili zako asubuhi, Kwa maana nimekutumaini Wewe. Unijulishe njia nitakayoiendea, Kwa maana nakuinulia nafsi yangu. 9 Ee Bwana, uniponye na adui zangu; Nimekukimbilia Wewe, unifiche. 10 Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, Kwa maana ndiwe Mungu wangu; Roho yako mwema aniongoze kwenye nchi sawa, 11 Ee Bwana, unihuishe kwa ajili ya jina lako, Kwa haki yako unitoe roho yangu taabuni; 12 Kwa fadhili zako utawakatilia mbali adui zangu; Na kuwaangamiza wote wanitesao nafsi, Kwa maana mimi ni mtumishi wako.

Zaburi 144

1 Na ahimidiwe Bwana, mwamba wangu, Anifundishaye mikono yangu vita, Vidole vyangu kupigana. 2 Mhisani wangu na boma langu, Ngome yangu na mwokozi wangu, Ngao yangu niliyemkimbilia, Huwatiisha watu wangu chini yangu. 3 Ee Bwana, mtu ni kitu gani hata umjue? Na binadamu hata umwangalie? 4 Binadamu amefanana na ubatili, Siku zake ni kama kivuli kipitacho. 5 Bwana, uziinamishe mbingu zako, ushuke, Uiguse milima nayo itatoka moshi. 6 Utupe umeme, uwatawanye, Uipige mishale yako, uwafadhaishe. 7 Uinyoshe mikono yako toka juu, uniponye, Unitoe katika maji mengi, katika mkono wa wageni. 8 Vinywa vyao vyasema visivyofaa, Na mkono wao wa kuume ni mkono wa uongo. 9 Ee Mungu, nitakuimbia wimbo mpya, Kwa kinanda chenye nyuzi kumi nitakuimbia. 10 Awapaye wafalme wokovu, Amwokoa Daudi, mtumishi wake, na upanga wa uovu. 11 Uniponye, unitoe, Katika mkono wa wageni. Vinywa vyao vyasema visivyofaa, Na mkono wao wa kuume ni mkono wa uongo. 12 Wana wetu na wawe kama miche Waliokua ujanani. Binti zetu kama nguzo za pembeni Zilizonakishwa kwa kupamba hekalu. 13 Ghala zetu na zijae Zenye akiba za jinsi zote. Kondoo zetu na wazae Elfu na makumi elfu mashambani mwetu. 14 Ng'ombe zetu na wachukue mizigo, Kusiwe na kushambuliwa. Wala kusiwe na kuhamishwa, Wala malalamiko katika njia zetu. 15 Heri watu wenye hali hiyo, Heri watu wenye Bwana kuwa Mungu wao.

Zaburi 145

1 Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, Nitalihimidi jina lako milele na milele. 2 Kila siku nitakuhimidi, Nitalisifu jina lako milele na milele. 3 Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana, Wala ukuu wake hautambulikani. 4 Kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako, Kitayatangaza matendo yako makuu. 5 Nitaifikiri fahari ya utukufu wa adhama yako, Na matendo yako yote ya ajabu. 6 Watu watayataja matendo yako ya kutisha, Nami nitausimulia ukuu wako. 7 Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu. Wataiimba haki yako. 8 Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, 9 Bwana ni mwema kwa watu wote, Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. 10 Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru, Na wacha Mungu wako watakuhimidi. 11 Wataunena utukufu wa ufalme wako, Na kuuhadithia uweza wako. 12 Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu, Na utukufu wa fahari ya ufalme wake. 13 Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote, Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote. 14 Bwana huwategemeza wote waangukao, Huwainua wote walioinama chini. 15 Macho ya watu wote yakuelekea Wewe, Nawe huwapa chakula chao wakati wake. 16 Waufumbua mkono wako, Wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake. 17 Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote, Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote. 18 Bwana yu karibu na wote wamwitao, Wote wamwitao kwa uaminifu. 19 Atawafanyia wamchao matakwa yao, Naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa. 20 Bwana huwahifadhi wote wampendao, Na wote wasio haki atawaangamiza. 21 Kinywa changu kitazinena sifa za Bwana; Wote wenye mwili na walihimidi jina lake takatifu milele na milele.

Zaburi 146

1 Haleluya. Ee nafsi yangu, umsifu Bwana. 2 Nitamsifu Bwana muda ninaoishi, Nitamwimbia Mungu wangu ningali ni hai. 3 Msiwatumainie wakuu, Wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake. 4 Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, Siku hiyo mawazo yake yapotea. 5 Heri ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, Na tumaini lake ni kwa Bwana, Mungu wake, 6 Aliyezifanya mbingu na nchi, Bahari na vitu vyote vilivyomo. Huishika kweli milele, 7 Huwafanyia hukumu walioonewa, Huwapa wenye njaa chakula; Bwana hufungua waliofungwa; 8 Bwana huwafumbua macho waliopofuka; Bwana huwainua walioinama; Bwana huwapenda wenye haki; 9 Bwana huwahifadhi wageni; Huwategemeza yatima na mjane; Bali njia ya wasio haki huipotosha. 10 Bwana atamiliki milele, Mungu wako, Ee Sayuni, kizazi hata kizazi. Haleluya.

Zaburi 147

1 Haleluya. Msifuni Bwana; Maana ni vema kumwimbia Mungu wetu, Maana kwapendeza, kusifu ni kuzuri. 2 Bwana ndiye aijengaye Yerusalemu, Huwakusanya waliotawanyika wa Israeli. 3 Huwaponya waliopondeka moyo, Na kuziganga jeraha zao. 4 Huihesabu idadi ya nyota, Huzipa zote majina. 5 Bwana wetu ni mkuu na mwingi wa nguvu, Akili zake hazina mpaka. 6 Bwana huwategemeza wenye upole, Huwaangusha chini wenye jeuri. 7 Mwimbieni Bwana kwa kushukuru, Mwimbieni Mungu wetu kwa kinubi. 8 Huzifunika mbingu kwa mawingu, Huitengenezea nchi mvua, Na kuyameesha majani milimani. 9 Humpa mnyama chakula chake, Wana-kunguru waliao. 10 Hapendezwi na nguvu za farasi, Wala hairidhii miguu ya mtu. 11 Bwana huwaridhia wao wamchao, Na kuzitarajia fadhili zake. 12 Msifu Bwana, Ee Yerusalemu; Msifu Mungu wako, Ee Sayuni. 13 Maana ameyakaza mapingo ya malango yako, Amewabariki wanao ndani yako. 14 Ndiye afanyaye amani mipakani mwako, Akushibishaye kwa unono wa ngano. 15 Huipeleka amri yake juu ya nchi, Neno lake lapiga mbio sana. 16 Ndiye atoaye theluji kama sufu, Huimwaga barafu yake kama majivu, 17 Hutupa mvua ya mawe kama makombo, Mbele ya baridi yake ni nani awezaye kusimama? 18 Hulituma neno lake na kuviyeyusha, Huuvumisha upepo wake, maji yakatiririka. 19 Humhubiri Yakobo neno lake, Na Israeli amri zake na hukumu zake. 20 Hakulitendea taifa lo lote mambo kama hayo, Wala hukumu zake hawakuzijua. Haleluya.

Zaburi 148

1 Haleluya. Msifuni Bwana kutoka mbinguni; Msifuni katika mahali palipo juu. 2 Msifuni, enyi malaika wake wote; Msifuni, majeshi yake yote. 3 Msifuni, jua na mwezi; Msifuni, nyota zote zenye mwanga. 4 Msifuni, enyi mbingu za mbingu, Nanyi maji mlioko juu ya mbingu. 5 Na vilisifu jina la Bwana, Kwa maana aliamuru, vikaumbwa. 6 Amevithibitisha hata milele na milele, Ametoa amri wala haitapita. 7 Msifuni Bwana kutoka nchi, Enyi nyangumi na vilindi vyote. 8 Moto na mvua ya mawe, theluji na mvuke, Upepo wa dhoruba ulitendao neno lake. 9 Milima na vilima vyote, Miti yenye matunda na mierezi yote. 10 Hayawani, na wanyama wafugwao, Vitambaavyo, na ndege wenye mbawa. 11 Wafalme wa dunia, na watu wote, Wakuu, na makadhi wote wa dunia. 12 Vijana waume, na wanawali, Wazee, na watoto; 13 Na walisifu jina la Bwana, Maana jina lake peke yake limetukuka; Adhama yake i juu ya nchi na mbingu. 14 Naye amewainulia watu wake pembe, Sifa za watauwa wake wote; Wana wa Israeli, watu walio karibu naye. Haleluya.

Zaburi 149

1 Haleluya. Mwimbieni Bwana wimbo mpya, Sifa zake katika kusanyiko la watauwa. 2 Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya, Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wao. 3 Na walisifu jina lake kwa kucheza, Kwa matari na kinubi wamwimbie. 4 Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake, Huwapamba wenye upole kwa wokovu. 5 Watauwa na waushangilie utukufu, Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao. 6 Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao, Na upanga mkali kuwili mikononi mwao. 7 Ili kufanya kisasi juu ya mataifa, Na adhabu juu ya kabila za watu. 8 Wawafunge wafalme wao kwa minyororo, Na wakuu wao kwa pingu za chuma. 9 Kuwafanyia hukumu iliyoandikwa; Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wake wote. Haleluya.

Zaburi 150

1 Haleluya. Msifuni Mungu katika patakatifu pake; Msifuni katika anga la uweza wake. 2 Msifuni kwa matendo yake makuu; Msifuni kwa kadiri ya wingi wa ukuu wake. 3 Msifuni kwa mvumo wa baragumu; Msifuni kwa kinanda na kinubi; 4 Msifuni kwa matari na kucheza; Msifuni kwa zeze na filimbi; 5 Msifuni kwa matoazi yaliayo; Msifuni kwa matoazi yavumayo sana. 6 Kila mwenye pumzi na amsifu Bwana. Haleluya.

Mithali 1

1 Mithali za Sulemani, mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli. 2 Kujua hekima na adabu; kutambua maneno ya ufahamu; 3 kufundishwa matendo ya busara, katika haki na hukumu na adili. 4 Kuwapa wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari; 5 mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu, na mwenye ufahamu ayafikie mashauri yenye njia. 6 Kufahamu mithali na kitendawili, na maneno ya wenye hekima na mafumbo yao. 7 Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu. 8 Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako, 9 Kwa maana hayo yatakuwa kilemba cha neema kichwani pako, Na mikufu shingoni mwako. 10 Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, Wewe usikubali. 11 Wakisema, Haya! Njoo pamoja nasi, Na tuvizie ili kumwaga damu; Tumwotee asiye na hatia, bila sababu; 12 Tuwameze hai kama kuzimu, Na wazima, kama wao washukao shimoni. 13 Tutapata mali yote ya thamani, Tutazijaza nyumba zetu mateka. 14 Wewe utashirikiana nasi; Tutakuwa na vitu vyote shirika. 15 Mwanangu, usiende njiani pamoja nao; Uzuie mguu wako usiende katika mapito yao. 16 Maana miguu yao huenda mbio maovuni, Nao hufanya haraka ili kumwaga damu. 17 Kwa kuwa mtego hutegwa bure, Mbele ya macho ya ndege ye yote. 18 Na hao hujiotea damu yao wenyewe, Hujinyemelea nafsi zao wenyewe. 19 Ndivyo zilivyo njia za kila mwenye tamaa ya mali; Huuondoa uhai wao walio nayo. 20 Hekima hupaza sauti yake katika njia kuu, Hutoa sauti yake katika viwanja; 21 Hulia penye mikutano mikubwa ya watu, Mahali pa kuyaingilia malango, Ndani ya mji hutamka maneno yake. 22 Enyi wajinga, hata lini mtapenda ujinga? Na wenye dharau kupenda dharau yao, Na wapumbavu kuchukia maarifa? 23 Geukeni kwa ajili ya maonyo yangu; Tazama, nitawamwagia roho yangu, Na kuwajulisheni maneno yangu. 24 Kwa kuwa nimeita, nanyi mkakataa; Nimeunyosha mkono wangu, asiangalie mtu; 25 Bali mmebatilisha shauri langu, Wala hamkutaka maonyo yangu; 26 Mimi nami nitacheka siku ya msiba wenu, Nitadhihaki hofu yenu ifikapo; 27 Hofu yenu ifikapo kama tufani, Na msiba wenu ufikapo kama kisulisuli, Dhiki na taabu zitakapowafikia. 28 Ndipo watakaponiita, lakini sitaitika; Watanitafuta kwa bidii, wasinione. 29 Kwa kuwa walichukia maarifa, Wala hawakuchagua kumcha Bwana. 30 Hawakukubali mashauri yangu, Wakayadharau maonyo yangu yote. 31 Kwa hiyo watakula matunda ya njia yao, Watashiba mashauri yao wenyewe. 32 Maana kurudi nyuma kwao wajinga kutawaua, Na kufanikiwa kwao wapumbavu kutawaangamiza. 33 Bali kila anisikilizaye atakaa salama, Naye atatulia bila kuogopa mabaya.

Mithali 2

1 Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, Na kuyaweka akiba maagizo yangu; 2 Hata ukatega sikio lako kusikia hekima, Ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; 3 Naam, ukiita busara, Na kupaza sauti yako upate ufahamu; 4 Ukiutafuta kama fedha, Na kuutafutia kama hazina iliyositirika; 5 Ndipo utakapofahamu kumcha Bwana, Na kupata kumjua Mungu. 6 Kwa kuwa Bwana huwapa watu hekima; Kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu; 7 Huwawekea wanyofu akiba ya hekima kamili; Yeye ni ngao kwao waendao kwa ukamilifu; 8 Apate kuyalinda mapito ya hukumu, Na kuhifadhi njia ya watakatifu wake. 9 Ndipo utakapofahamu haki na hukumu, Na adili, na kila njia njema. 10 Maana hekima itaingia moyoni mwako, Na maarifa yatakupendeza nafsi yako; 11 Busara itakulinda; Ufahamu utakuhifadhi. 12 Ili kukuokoa na njia ya uovu, Na watu wanenao yaliyopotoka; 13 Watu waziachao njia za unyofu, Ili kuziendea njia za giza; 14 Wafurahio kutenda mabaya; Wapendezwao na upotoe wa waovu; 15 Waliopotoka katika njia zao; Walio wakaidi katika mapito yao. 16 Ili kuokoka na malaya, Naam, malaya mwenye kubembeleza kwa maneno yake; 17 Amwachaye rafiki wa ujana wake, Na kulisahau agano la Mungu wake. 18 Maana nyumba yake inaelekea mauti, Na mapito yake yanakwenda kwenye wafu. 19 Katika hao wamwendeao harudi hata mmoja, Wala hawazifikilii njia za uzima. 20 Ili upate kwenda katika njia ya watu wema, Na kuyashika mapito ya wenye haki. 21 Maana wanyofu watakaa katika nchi, Na wakamilifu watadumu ndani yake. 22 Bali waovu watatengwa na nchi, Nao wafanyao hila watang'olewa.

Mithali 3

1 Mwanangu, usiisahau sheria yangu, Bali moyo wako uzishike amri zangu. 2 Maana zitakuongezea wingi wa siku. Na miaka ya uzima, na amani. 3 Rehema na kweli zisifarakane nawe; Zifunge shingoni mwako; Ziandike juu ya kibao cha moyo wako. 4 Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri, Mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu. 5 Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; 6 Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. 7 Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu. 8 Itakuwa afya mwilini pako, Na mafuta mifupani mwako. 9 Mheshimu Bwana kwa mali yako, Na kwa malimbuko ya mazao yako yote. 10 Ndipo ghala zako zitakapojazwa kwa wingi, Na mashinikizo yako yatafurika divai mpya. 11 Mwanangu, usidharau kuadhibiwa na Bwana, Wala usione ni taabu kurudiwa naye. 12 Kwa kuwa Bwana ampendaye humrudi, Kama vile baba mwanawe ampendezaye. 13 Heri mtu yule aonaye hekima, Na mtu yule apataye ufahamu. 14 Maana biashara yake ni bora kuliko biashara ya fedha, Na faida yake ni nyingi kuliko dhahabu safi. 15 Yeye ana thamani kuliko marijani, Wala vyote uvitamanivyo havilingani naye. 16 Ana wingi wa siku katika mkono wake wa kuume, Utajiri na heshima katika mkono wake wa kushoto. 17 Njia zake ni njia za kupendeza sana, Na mapito yake yote ni amani. 18 Yeye ni mti wa uzima kwao wamshikao sana; Ana heri kila mtu ashikamanaye naye. 19 Kwa hekima Bwana aliiweka misingi ya nchi; Kwa akili zake akazifanya mbingu imara; 20 Kwa maarifa yake vilindi viligawanyika; Na mawingu yadondoza umande. 21 Mwanangu, yasiondoke haya machoni pako, Shika hekima kamili na busara. 22 Basi yatakuwa uzima kwa nafsi yako, Na neema shingoni mwako. 23 Ndipo utakapokwenda katika njia yako salama, Wala mguu wako hautakwaa. 24 Ulalapo hutaona hofu; Naam, utalala na usingizi wako utakuwa mtamu. 25 Usiogope hofu ya ghafula, Wala uharibifu wa waovu utakapofika. 26 Kwa kuwa Bwana atakuwa tumaini lako, Naye atakulinda mguu wako usinaswe. 27 Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, Ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda. 28 Usimwambie jirani yako, Nenda, urudi halafu, na kesho nitakupa; Nawe unacho kitu kile karibu nawe. 29 Usiwaze mabaya juu ya jirani yako, Ambaye anakaa karibu nawe na kujiona salama. 30 Usishindane na mtu bila sababu, Ikiwa hakukudhuru kwa lo lote. 31 Usimhusudu mtu mwenye jeuri, Wala usiichague mojawapo ya njia zake. 32 Maana mtu mkaidi ni chukizo kwa Bwana, Bali siri yake ni pamoja na wanyofu. 33 Laana ya Bwana i katika nyumba ya waovu, Bali huibariki maskani ya mwenye haki. 34 Hakika yake huwadharau wenye dharau, Bali huwapa wanyenyekevu neema. 35 Wenye hekima wataurithi utukufu, Bali kukuzwa kwa wapumbavu ni fedheha.

Mithali 4

1 Wanangu, yasikilizeni mausia ya baba yenu, Tegeni masikio mpate kujua ufahamu. 2 Kwa kuwa nawapa mafundisho mazuri; Msiiache sheria yangu. 3 Maana nalikuwa mwana kwa baba yangu, Mpole, mpenzi wa pekee wa mama yangu. 4 Naye akanifundisha, akaniambia, Moyo wako uyahifadhi maneno yangu; Shika amri zangu ukaishi. 5 Jipatie hekima, jipatie ufahamu; usiusahau; Wala usiyakatae maneno ya kinywa changu. 6 Usimwache, naye atakuhifadhi; Umpende, naye atakulinda. 7 Bora hekima, basi jipatie hekima; Naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu. 8 Umtukuze, naye atakukuza; Atakupatia heshima, ukimkumbatia. 9 Atakupa neema kuwa kilemba kichwani; Na kukukirimia taji ya uzuri. 10 Mwanangu, sikiliza, na kuzipokea kauli zangu; Na miaka ya maisha yako itakuwa mingi. 11 Nimekufundisha katika njia ya hekima; Nimekuongoza katika mapito ya unyofu. 12 Uendapo, hatua zako hazitadhiikika, Wala ukipiga mbio hutajikwaa. 13 Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; Mshike, maana yeye ni uzima wako. 14 Usiingie katika njia ya waovu, Wala usitembee katika njia ya wabaya. 15 Jiepushe nayo, usipite karibu nayo, Igeukie mbali, ukaende zako. 16 Maana hawalali isipokuwa wametenda madhara; Huondolewa usingizi, ikiwa hawakumwangusha mtu. 17 Maana wao hula mkate wa uovu, Nao hunywa divai ya jeuri. 18 Bali njia ya wenye haki ni kama nuru ing'aayo, Ikizidi kung'aa hata mchana mkamilifu. 19 Njia ya waovu ni kama giza; Hawajui ni kitu gani kiwakwazacho. 20 Mwanangu, sikiliza maneno yangu; Tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. 21 Zisiondoke machoni pako; Uzihifadhi ndani ya moyo wako. 22 Maana ni uhai kwa wale wazipatao, Na afya ya mwili wao wote. 23 Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; Maana ndiko zitokako chemchemi za uzima. 24 Kinywa cha ukaidi ukitenge nawe, Na midomo ya upotovu uiweke mbali nawe. 25 Macho yako yatazame mbele, Na kope zako zitazame mbele yako sawasawa. 26 Ulisawazishe pito la mguu wako, Na njia zako zote zithibitike; 27 Usigeuke kwa kuume wala kwa kushoto; Ondoa mguu wako maovuni.

Mithali 5

1 Mwanangu, sikiliza hekima yangu; Tega sikio lako, mzisikie akili zangu; 2 Upate kuilinda busara, Na midomo yako iyahifadhi maarifa. 3 Maana midomo ya malaya hudondoza asali, Na kinywa chake ni laini kuliko mafuta; 4 Lakini mwisho wake ni mchungu kuliko pakanga; Ni mkali kama upanga wa makali kuwili. 5 Miguu yake inatelemkia mauti; Hatua zake zinashikamana na kuzimu; 6 Hata asiweze kuiona njia sawa ya uzima; Njia zake ni za kutanga-tanga wala hana habari. 7 Basi, wanangu, nisikilizeni sasa, Wala msiache maneno ya kinywa changu. 8 Itenge njia yako mbali naye, Wala usiukaribie mlango wa nyumba yake. 9 Usije ukawapa wengine heshima yako, Na wakorofi miaka yako; 10 Wageni wasije wakashiba nguvu zako; Kazi zako zikawa ndani ya nyumba ya mgeni; 11 Nawe ukaziombolea siku zako za mwisho, Nyama yako na mwili wako utakapoangamia; 12 Ukasema, Jinsi nilivyochukia maonyo, Na moyo wangu ukadharau kukemewa; 13 Wala sikuisikia sauti ya waalimu wangu, Wala sikuwategea sikio langu walionifundisha! 14 Nalikuwa karibu na kuingia katika maovu yote, Katikati ya mkutano na kusanyiko. 15 Unywe maji ya birika lako mwenyewe, Na maji yenye kububujika katika kisima chako. 16 Je! Chemchemi zako zitawanyike mbali, Na mito ya maji katika njia kuu? 17 Yawe yako mwenyewe peke yako, Wala si ya wageni pamoja nawe. 18 Chemchemi yako ibarikiwe; Nawe umfurahie mke wa ujana wako. 19 Ni ayala apendaye na paa apendezaye; Maziwa yake yakutoshe sikuzote; Na kwa upendo wake ushangilie daima. 20 Mwanangu! Mbona unashangilia malaya, Na kukikumbatia kifua cha mgeni? 21 Kwa maana njia za mwanadamu zi mbele za macho ya Bwana, Na mienendo yake yote huitafakari. 22 Maovu yake yeye yatampata mdhalimu, Naye atashikwa kwa kamba za dhambi zake. 23 Atakufa huyo kwa kukosa maonyo, Naye atapotea kwa wingi wa ujinga wake.

Mithali 6

1 Mwanangu, kama umekuwa mdhamini wa rafiki yako, Ikiwa wewe na mgeni mmepana mikono, 2 Basi umetegwa kwa maneno ya kinywa chako, Umekamatwa kwa maneno ya kinywa chako, 3 Sasa, mwanangu, fanya hivi ukajiokoe, Kwa kuwa umejitia mkononi mwa jirani yako; Nenda ukanyenyekee, na kumsihi jirani yako. 4 Usiache macho yako kupata usingizi, Wala kope za macho yako kusinzia. 5 Ujiponye kama paa na mkono wa mwindaji, Na kama ndege katika mkono wa mtega mitego. 6 Ewe mvivu, mwendee chungu, Zitafakari njia zake ukapate hekima. 7 Kwa maana yeye hana akida, Wala msimamizi, wala mkuu, 8 Lakini hujiwekea akiba ya chakula wakati wa jua; Hukusanya chakula chake wakati wa mavuno. 9 Ewe mvivu, utalala hata lini? Utaondoka lini katika usingizi wako? 10 Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, Bado kukunja mikono upate usingizi! 11 Hivyo umaskini wako huja kama mnyang'anyi, Na uhitaji wako kama mtu mwenye silaha. 12 Mtu asiyefaa kitu, mtu wa uovu; Huenda njiani mwenye kinywa cha upotofu. 13 Hukonyeza kwa macho, hunena kwa miguu, Huwaashiria watu kwa vidole vyake. 14 Mna upotofu moyoni mwake, hutunga uovu daima, Hupanda mbegu za magomvi. 15 Basi msiba utampata kwa ghafula; Ghafula atavunjika, bila njia ya kupona. 16 Kuna vitu sita anavyovichukia Bwana; Naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. 17 Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, Na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; 18 Moyo uwazao mawazo mabaya; Miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; 19 Shahidi wa uongo asemaye uongo; Naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu. 20 Mwanangu, shika maagizo ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako. 21 Yafunge hayo katika moyo wako daima; Jivike hayo shingoni mwako. 22 Uendapo yatakuongoza, ulalapo yatakulinda, Na uamkapo yatazungumza nawe. 23 Maana maagizo hayo ni taa, na sheria hiyo ni nuru, Na maonyo ya kumwadilisha mtu ni njia ya uzima. 24 Yakulinde na mwanamke mwovu, asikupate, Na kukuponya na ubembelezi wa mgeni. 25 Usiutamani uzuri wake moyoni mwako; Wala usikubali akunase kwa kope za macho yake. 26 Maana kwa malaya mtu hutiwa katika hali ya kuhitaji kipande cha mkate; Na kahaba humwinda mtu anase nafsi yake iliyo ya thamani 27 Je! Mtu aweza kuua moto kifuani pake, Na nguo zake zisiteketezwe? 28 Je! Mtu aweza kukanyaga makaa ya moto, Na nyayo zake zisiungue? 29 Ndivyo alivyo aingiaye kwa mke wa jirani yake; Kila mtu amgusaye huyo atakuwa na hatia. 30 Watu hawamdharau mwivi, Akiiba ili kujishibisha, iwapo aona njaa; 31 Lakini akipatikana, atalipa mara saba; Atatoa mali yote ya nyumba yake. 32 Mtu aziniye na mwanamke hana akili kabisa; Afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake. 33 Atapata jeraha na kuvunjiwa heshima; Wala fedheha yake haitafutika. 34 Maana wivu ni ghadhabu ya mtu; Wala hatahurumia siku ya kujilipiza kisasi. 35 Hatakubali ukombozi uwao wote; Wala hatakuwa radhi, ujapomlipa vitu vingi.

Mithali 7

1 Mwanangu, yashike maneno yangu, Na kuziweka amri zangu akiba kwako. 2 Uzishike amri zangu ukaishi, Na sheria yangu kama mboni ya jicho lako. 3 Zifunge katika vidole vyako; Ziandike juu ya kibao cha moyo wako. 4 Mwambie hekima, Wewe ndiwe umbu langu; Mwite ufahamu jamaa yako mwanamke. 5 Wapate kukulinda na malaya, Na mgeni akubembelezaye kwa maneno yake. 6 Maana katika dirisha la nyumba yangu Nalichungulia katika shubaka yake; 7 Nikaona katikati ya wajinga, Nikamtambua miongoni mwa vijana, Kijana mmoja asiyekuwa na akili, 8 Akipita njiani karibu na pembe yake, Akiishika njia iendayo nyumbani kwake, 9 Wakati wa magharibi, wakati wa jioni, Usiku wa manane, gizani. 10 Na tazama, mwanamke akamkuta, Ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo; 11 Ana kelele, na ukaidi; Miguu yake haikai nyumbani mwake. 12 Mara yu katika njia kuu, mara viwanjani, Naye huotea kwenye pembe za kila njia. 13 Basi akamshika, akambusu, Akamwambia kwa uso usio na haya, 14 Kwangu ziko sadaka za amani; Leo hivi nimeziondoa nadhiri zangu; 15 Ndiyo maana nikatoka nikulaki, Nikutafute uso wako kwa bidii, nami nimekuona. 16 Nimetandika kitanda changu, magodoro mazuri, Kwa matandiko ya Kimisri yenye mistari. 17 Nimetia kitanda changu manukato, Manemane na udi na mdalasini. 18 Haya, na tushibe upendo hata asubuhi, Tujifurahishe nafsi zetu kwa mahaba. 19 Maana mume wangu hayumo nyumbani, Amekwenda safari ya mbali; 20 Amechukua mfuko wa fedha mkononi; Atarudi wakati wa mwezi mpevu. 21 Kwa maneno yake mengi na ulaini akamshawishi, Kwa ubembelezi wa midomo yake akamshinda. 22 Huyo akafuatana naye mara hiyo, Kama vile ng'ombe aendavyo machinjoni; Au mpumbavu kuadhibiwa katika pingu; 23 Hata mshale umchome maini; Kama ndege aendaye haraka mtegoni; Wala hajui ya kuwa ni hasara ya nafsi yake. 24 Basi, wanangu, nisikilizeni sasa, Mkayaangalie maneno ya kinywa changu. 25 Moyo wako usizielekee njia zake, Wala usipotee katika mapito yake. 26 Maana amewaangusha wengi waliojeruhi, Naam, jumla ya waliouawa naye ni jeshi kubwa. 27 Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, Hushuka mpaka vyumba vya mauti.

Mithali 8

1 Je! Hekima halii? Ufahamu hatoi sauti yake? 2 Juu ya mahali palipoinuka karibu na njia, Penye njia panda, ndipo asimamapo. 3 Karibu na malango, mahali pa kuingia mjini, Mahali pa kuyaingilia malango anapiga kelele. 4 Enyi watu, nawaita ninyi; Na sauti yangu ni kwa wanadamu. 5 Enyi wajinga, fahamuni werevu, Nanyi wapumbavu, mpate moyo wa kufahamu. 6 Sikieni, maana nitasema yaliyo mazuri, Na kufumbua midomo yangu kutakuwa maadili. 7 Maana kinywa changu kitasema kweli, Na uovu ni chukizo kwa midomo yangu. 8 Maneno yote ya kinywa changu yana haki; Hapana hata neno lililopotoka au la ukaidi. 9 Yote humwelea yule afahamuye, Yote huelekea mbele yao waliopata maarifa. 10 Pokea mafundisho yangu, wala si fedha, Na maarifa kuliko dhahabu safi. 11 Maana hekima ni bora kuliko marijani; Wala vyote vinavyotamanika havilingani nayo. 12 Mimi, hekima, nimefanya werevu kuwa kao langu; Natafuta maarifa na busara. 13 Kumcha Bwana ni kuchukia uovu; Kiburi na majivuno, na njia mbovu, Na kinywa cha ukaidi pia nakichukia. 14 Shauri ni langu, na maarifa yaliyo sahihi; Mimi ni ufahamu, mimi nina nguvu. 15 Kwa msaada wangu wafalme humiliki, Na wakuu wanahukumu haki. 16 Kwa msaada wangu wakuu hutawala, Na waungwana, naam, waamuzi wote wa dunia. 17 Nawapenda wale wanipendao, Na wale wanitafutao kwa bidii wataniona. 18 Utajiri na heshima ziko kwangu, Naam, utajiri udumuo, na haki pia. 19 Matunda yangu hupita dhahabu, naam, dhahabu safi, Na faida yangu hupita fedha iliyo teule. 20 Natembea katika njia ya haki, Katikati ya mapito ya hukumu. 21 Niwarithishe mali wale wanipendao, Tena nipate kuzijaza hazina zao. 22 Bwana alikuwa nami katika mwanzo wa njia yake, Kabla ya matendo yake ya kale. 23 Nalitukuka tokea milele, tangu awali, Kabla haijawako dunia. 24 Wakati visipokuwako vilindi nalizaliwa, Wakati zisipokuwako chemchemi zilizojaa maji. 25 Kabla milima haijawekwa imara, Kabla ya vilima nalizaliwa. 26 Alipokuwa hajaiumba dunia, wala makonde Wala chanzo cha mavumbi ya dunia; 27 Alipozithibitisha mbingu nalikuwako; Alipopiga duara katika uso wa bahari; 28 Alipofanya imara mawingu yaliyo juu; Chemchemi za bahari zilipopata nguvu; 29 Alipoipa bahari mpaka wake, Kwamba maji yake yasiasi amri yake; Alipoiagiza misingi ya nchi; 30 Ndipo nilipokuwa pamoja naye, kama stadi wa kazi; Nikawa furaha yake kila siku; Nikifurahi daima mbele zake; 31 Nikiifurahia dunia inayokaliwa na watu; Na furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu. 32 Basi, wanangu, nisikilizeni sasa; Maana heri hao wazishikao amri zangu. 33 Sikieni mafundisho, mpate hekima, Wala msiikatae. 34 Ana heri mtu yule anisikilizaye, Akisubiri sikuzote malangoni pangu, Akingoja penye vizingiti vya milango yangu. 35 Maana yeye anionaye mimi aona uzima, Naye atapata kibali kwa Bwana. 36 Bali anikosaye hujidhuru nafsi yake mwenyewe, Na wao wanichukiao hupenda mauti.

Mithali 9

1 Hekima umeijenga nyumba yake, Amezichonga nguzo zake saba; 2 Amechinja nyama zake, umechanganya divai yake, Ameiandalia meza yake pia. 3 Amewatuma wajakazi wake, analia, Mahali pa mjini palipoinuka sana, 4 Kila aliye mjinga na aingie humu. Tena amwambia mtu aliyepungukiwa na akili, 5 Njoo ule mkate wangu, Ukanywe divai niliyoichanganya. 6 Enyi wajinga, acheni ujinga, mkaishi, Mkaende katika njia ya ufahamu. 7 Amkemeaye mwenye dharau hujipatia fedheha; Amkaripiaye mtu mbaya hujipatia aibu. 8 Usimkaripie mwenye dharau, asije akakuchukia; Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda. 9 Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima; Mfundishe mwenye haki, naye atazidi kuwa na elimu; 10 Kumcha Bwana ni mwanzo wa hekima; Na kumjua Mtakatifu ni ufahamu. 11 Maana, kwa msaada wangu siku zako zitazidishwa; Na miaka ya maisha yako itaongezwa. 12 Kama una hekima, una hekima kwa nafsi yako; Na kama una dharau, utaichukua peke yako. 13 Mwanamke mpumbavu hupiga kelele, Ni mjinga, hajui kitu. 14 Hukaa mlangoni pa nyumba yake, Juu ya kiti mahali pa mjini palipoinuka, 15 Apate kuwaita wapitao njiani, Waendao moja kwa moja katika njia zao. 16 Kila aliye mjinga na aingie humu. Tena amwambia mtu aliyepungukiwa na akili, 17 Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza. 18 Lakini huyo hajui ya kuwa wafu wamo humo; Ya kuwa wageni wake wamo chini kuzimuni.

Mithali 10

1 Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye. 2 Hazina za uovu hazifaidii kitu; Bali haki huokoa na mauti. 3 Bwana hataiacha nafsi ya mwenye haki ife na njaa; Bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali. 4 Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini; Bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha. 5 Akusanyaye wakati wa hari ni mwana mwenye hekima; Bali asinziaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha. 6 Baraka humkalia mwenye haki kichwani; Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu. 7 Kuwakumbuka wenye haki huwa na baraka; Bali jina la mtu mwovu litaoza. 8 Aliye na akili moyoni mwake atapokea agizo; Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka. 9 Aendaye kwa unyofu huenda salama; Bali apotoshaye njia zake atajulikana. 10 Akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko; Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka. 11 Kinywa chake mwenye haki ni chemchemi ya uzima; Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu, 12 Kuchukiana huondokesha fitina; Bali kupendana husitiri makosa yote. 13 Hekima hupatikana midomoni mwa mwenye ufahamu; Bali fimbo hufaa kwa mgongo wake asiye na ufahamu. 14 Watu wenye akili huweka akiba ya maarifa; Bali kinywa cha mpumbavu ni uangamivu ulio karibu. 15 Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; Uangamivu wa maskini ni umaskini wao. 16 Kazi yake mwenye haki huuelekea uzima; Mazao ya wabaya huuelekea dhambi. 17 Akubaliye kurudiwa huwa katika njia ya uzima; Bali yeye aachaye maonyo hukosa. 18 Yeye afichaye chuki ana midomo ya uongo, Na yeye asingiziaye ni mpumbavu. 19 Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; Bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili. 20 Ulimi wa mwenye haki ni kama fedha teule; Moyo wa mtu mbaya haufai kitu. 21 Midomo ya mwenye haki hulisha watu wengi; Bali wapumbavu hufa kwa kuwa hawana ufahamu. 22 Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo. 23 Kwa mpumbavu kutenda maovu ni kama mchezo; Bali mtu mwenye ufahamu ana hekima. 24 Aogopacho mtu asiye haki ndicho kitakachomjilia; Na wenye haki watapewa matakwa yao. 25 Kisulisuli kikiisha pita asiye haki hayuko tena; Bali mwenye haki ni msingi wa milele. 26 Kama siki menoni, na kama moshi machoni, Ndivyo alivyo mtu mvivu kwao wamtumao. 27 Kumcha Bwana kwaongeza siku za mtu; Bali miaka yao wasio haki itapunguzwa. 28 Matumaini yao wenye haki yatakuwa furaha; Bali kutaraji kwao wasio haki kutapotea. 29 Njia ya Bwana ni kimbilio lake mtu mkamilifu; Bali ni uharibifu kwao watendao maovu. 30 Mwenye haki hataondolewa milele; Bali wasio haki hawatakaa katika nchi. 31 Kinywa cha mwenye haki hutoa hekima; Bali ulimi wa ukaidi utakatiliwa mbali. 32 Midomo ya mwenye haki huyajua yatakayokubaliwa; Bali kinywa chao wasio haki hunena ukaidi.

Mithali 11

1 Mizani ya hadaa ni chukizo kwa Bwana; Bali vipimo vilivyo sawasawa humpendeza. 2 Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu. 3 Ukamilifu wao wenye haki utawaongoza Bali ukaidi wao wenye fitina utawaangamiza. 4 Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu; Bali haki huokoa na mauti. 5 Haki yake mtu mkamilifu itamwongoza njia yake; Bali mtu mwovu ataanguka kwa uovu wake. 6 Haki yao wenye haki itawaokoa; Bali wafanyao fitina watanaswa kwa hila yao wenyewe. 7 Mtu mwovu atakapokufa, taraja lake lapotea; Na matumaini ya uovu huangamia. 8 Mwenye haki huokolewa katika dhiki, Na mtu mwovu ataiingia badala yake. 9 Asiyemcha Mungu humpoteza jirani yake kwa kinywa chake; Bali wenye haki watapona kwa maarifa. 10 Wenye haki wasitawipo, mji hufurahi; Waovu waangamiapo, watu hupiga kelele. 11 Mji hutukuzwa kwa mbaraka wa mwenye haki; Bali mji hupinduliwa kwa kinywa cha mwovu. 12 Asiye na akili humdharau mwenziwe; Bali mtu aliye na ufahamu hunyamaza. 13 Mwenye kitango akisingizia hufunua siri; Bali mwenye roho ya uaminifu husitiri mambo. 14 Pasipo mashauri taifa huanguka; Bali kwa wingi wa washauri huja wokovu. 15 Amdhaminiye mgeni hakosi ataumia; Achukiaye mambo ya dhamana yu salama. 16 Mwanamke wa adabu huheshimiwa daima; Na watu wakali hushika mali siku zote. 17 Mwenye rehema huitendea mema nafsi yake; Aliye mkali hujisumbua mwili wake. 18 Mtu mwovu hupata mshahara wa udanganyifu; Apandaye haki ana thawabu ya hakika. 19 Haki huelekea uzima; Afuataye maovu hufuata mauti yake mwenyewe. 20 Wenye kuhalifu moyoni ni chukizo kwa Bwana; Walio wakamilifu katika njia zao humpendeza. 21 Hakika, mtu mwovu hatakosa adhabu; Bali wazao wa wenye haki wataokoka. 22 Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, Kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili. 23 Haja ya mwenye haki ni mema tu; Bali kutaraji kwake mtu mwovu ni ghadhabu. 24 Kuna atawanyaye, lakini huongezewa zaidi; Kuna azuiaye isivyo haki, lakini huelekea uhitaji. 25 Nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa; Anyweshaye atanyweshwa mwenyewe. 26 Awanyimaye watu nafaka, watu watamlaani; Auzaye nafaka, baraka itakuwa kichwani pake. 27 Atafutaye mema kwa bidii hutafuta fadhili; Atafutaye madhara, hayo yatamjia. 28 Azitegemeaye mali zake ataanguka; Mwenye haki atasitawi kama jani. 29 Ataabishaye nyumba yake mwenyewe ataurithi upepo; Mpumbavu atakuwa mtumwa wa mtu mwenye moyo wa akili. 30 Mazao ya mwenye haki ni mti wa uzima; Na mwenye hekima huvuta roho za watu. 31 Tazama, mwenye haki atalipwa duniani; Basi mwovu na mkosaji si mara nyingi zaidi?

Mithali 12

1 Kila apendaye mafundisho hupenda maarifa; Bali yeye achukiaye kulaumiwa ni kama mnyama. 2 Mtu mwema atapata upendeleo kwa Bwana; Bali mtu wa hila atahukumiwa naye. 3 Mtu hatathibitika kwa njia ya uovu; Shina la mwenye haki halitaondolewa kamwe. 4 Mwanamke mwema ni taji ya mumewe; Bali aaibishaye ni kama kuoza mifupani mwake. 5 Mawazo ya mwenye haki ni adili; Bali mashauri ya mtu mwovu ni hadaa. 6 Maneno ya waovu huotea damu; Bali kinywa cha wanyofu kitawaokoa. 7 Waovu huangamia, hata hawako tena; Bali nyumba ya mwenye haki itasimama. 8 Mtu atasifiwa kwa kadiri ya akili zake; Bali mwenye moyo wa ukaidi atadharauliwa. 9 Afadhali mtu anayedharauliwa, ikiwa ana mtumwa, Kuliko ajisifuye, ikiwa anahitaji chakula. 10 Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake; Bali huruma za mtu mwovu ni ukatili. 11 Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele; Bali afuataye mambo ya upuzi hana ufahamu. 12 Asiye haki hutamani nyavu za wabaya; Bali shina lao wenye haki huleta matunda. 13 Katika kosa la midomo kuna mtego kwa mbaya; Bali mwenye haki atatoka katika taabu. 14 Mtu atashiba mema kwa matunda ya kinywa chake; Na atarudishiwa matendo ya mikono yake. 15 Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; Bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri. 16 Ghadhabu ya mpumbavu hujulika mara; Bali mtu mwerevu husitiri aibu. 17 Atamkaye maneno ya kweli hufunua haki; Bali shahidi wa uongo hutamka hila. 18 Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; Bali ulimi wa mwenye haki ni afya. 19 Mdomo wa kweli utathibitishwa milele; Bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu. 20 Hila imo mioyoni mwao wafikirio uovu; Bali wafanyao mashauri ya amani, kwao kuna furaha. 21 Mwenye haki hatapatikana na msiba wo wote; Bali wasio haki watajazwa mabaya. 22 Midomo ya uongo ni chukizo kwa Bwana; Bali watendao uaminifu ndio furaha yake. 23 Mwanadamu mwenye busara husitiri maarifa; Bali moyo wa wapumbavu hutangaza upumbavu. 24 Mkono wa mwenye bidii utatawala; Bali mvivu atalipishwa kodi. 25 Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; Bali neno jema huufurahisha. 26 Mwenye haki ni kiongozi cha mwenzake; Bali njia ya wasio haki huwakosesha. 27 Mtu mvivu hapiki mawindo yake; Bali mwenye bidii anazo mali za thamani. 28 Katika njia ya haki kuna uhai; Wala hakuna mauti katika mapito yake.

Mithali 13

1 Mwana mwenye hekima husikiliza mausia ya babaye; Bali mwenye dharau hasikilizi maonyo. 2 Mtu atakula mema kwa matunda ya kinywa chake; Bali nafsi ya mtu haini itakula jeuri. 3 Yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; Bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu. 4 Nafsi ya mtu mvivu hutamani asipate kitu; Bali nafsi ya mwenye bidii itanenepeshwa. 5 Mwenye haki huchukia kusema uongo; Bali mtu mbaya huwa karaha, hupatwa na aibu. 6 Haki humlinda yeye aliye mnyofu katika njia yake; Bali ubaya humwangusha mwenye dhambi. 7 Kuna mtu mwenye kujitajirisha, lakini hana kitu; Kuna ajifanyaye kuwa maskini, lakini ana mali nyingi. 8 Dia ya nafsi ya mtu ni utajiri wake; Bali mtu maskini hasikii ogofyo lo lote. 9 Nuru ya mwenye haki yang'aa sana; Bali taa ya mtu mbaya itazimika. 10 Kiburi huleta mashindano tu; Bali hekima hukaa nao wanaoshauriana. 11 Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa. 12 Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima. 13 Kila alidharauye neno hujiletea uharibifu; Bali yeye aiogopaye amri atapewa thawabu. 14 Sheria ya mwenye akili ni chemchemi ya uzima, Ili kuepukana na tanzi za mauti. 15 Ufahamu mwema huleta upendeleo; Bali njia ya haini huparuza. 16 Kila aliye na busara hutenda kazi kwa maarifa; Bali mpumbavu hueneza upumbavu. 17 Mjumbe mbaya huanguka maovuni; Bali mjumbe mwaminifu ni afya. 18 Umaskini na fedheha zitampata yeye akataaye kurudiwa; Bali yeye aangaliaye maonyo ataheshimiwa. 19 Haja iliyopatikana ni tamu nafsini mwa mtu; Bali kujitenga na maovu ni chukizo kwa wapumbavu. 20 Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; Bali rafiki wa wapumbavu ataumia. 21 Uovu huwaandamia wenye dhambi; Bali mwenye haki atalipwa mema. 22 Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi; Na mali ya mkosaji huwa akiba kwa mwenye haki. 23 Chakula kingi chapatikana kwa ukulima wa maskini; Bali viko viharibiwavyo kwa sababu ya dhuluma. 24 Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; Bali yeye ampendaye humrudi mapema. 25 Mwenye haki hula akaishibisha nafsi yake; Bali tumbo la mtu mbaya litaona njaa.

Mithali 14

1 Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. 2 Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha Bwana; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau. 3 Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi. 4 Zizi ni safi ambapo hapana ng'ombe; Bali nguvu za ng'ombe zaleta faida nyingi. 5 Shahidi mwaminifu hatasema uongo; Bali shahidi wa uongo, pumzi zake ni uongo. 6 Mwenye dharau hutafuta hekima, asiipate; Bali maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu. 7 Toka mbele ya uso wa mpumbavu, Maana hutaona kwake midomo ya maarifa. 8 Akili za mwenye busara ni kujua njia yake; Lakini upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu. 9 Wapumbavu huidharau hatia; Bali upo upendeleo kwa wenye haki. 10 Moyo huujua uchungu wa nafsi yake, Wala mgeni haishiriki furaha yake. 11 Nyumba ya mtu mbaya itabomolewa; Bali hema ya mwenye haki itafanikiwa. 12 Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti. 13 Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo. 14 Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake. 15 Mjinga huamini kila neno; Bali mwenye busara huangalia sana aendavyo. 16 Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu; Bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai. 17 Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga; Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa. 18 Wajinga hurithi upumbavu; Bali wenye busara huvikwa taji ya maarifa. 19 Wabaya huinama mbele ya wema, Na wasio haki malangoni mwao wenye haki. 20 Maskini huchukiwa hata na jirani yake; Bali tajiri ana rafiki wengi. 21 Amdharauye mwenzake afanya dhambi; Bali amhurumiaye maskini ana heri. 22 Je! Hawakosi wawazao mabaya? Bali fadhili na kweli zina wao wawazao mema. 23 Katika kila kazi mna faida; Bali maneno ya midomo huleta hasara tu. 24 Taji ya wenye hekima ni mali zao; Bali upumbavu wa wajinga ni upumbavu tu. 25 Shahidi wa kweli huponya nafsi za watu; Bali atoaye uongo hudanganya. 26 Kumcha Bwana ni tumaini imara; Watoto wake watakuwa na kimbilio. 27 Kumcha Bwana ni chemchemi ya uzima, Ili kuepukana na tanzi za mauti. 28 Utukufu wa mfalme ni wingi wa watu wake; Bali uchache wa watu ni uharibifu wa mkuu wao. 29 Asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi; Bali mwenye roho ya hamaki hutukuza upumbavu. 30 Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili; Bali husuda ni ubovu wa mifupa. 31 Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; Bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu. 32 Mtu mbaya husukumwa chini katika kutenda mabaya kwake; Bali mwenye haki ana matumaini katika kufa kwake. 33 Hekima hukaa katika moyo wake mwenye ufahamu; Bali yaliyo ndani ya wapumbavu hudhihirika. 34 Haki huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote. 35 Upendeleo wa mfalme humwelekea mtumwa atendaye kwa busara; Bali ghadhabu yake itakuwa juu yake aletaye aibu.

Mithali 15

1 Jawabu la upole hugeuza hasira; Bali neno liumizalo huchochea ghadhabu. 2 Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri; Bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu. 3 Macho ya Bwana yako kila mahali; Yakimchunguza mbaya na mwema. 4 Ulimi safi ni mti wa uzima; Bali ukorofi wa ulimi huvunja moyo. 5 Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye; Bali yeye aangaliaye maonyo hupata busara. 6 Katika nyumba ya mwenye haki mna akiba nyingi; Bali mapato ya mtu mbaya huwa taabu tu. 7 Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa; Bali moyo wa mpumbavu haufanyi hivyo. 8 Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake. 9 Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana; Bali humpenda mtu afuatiaye wema. 10 Adhabu kali ina yeye aiachaye njia; Naye achukiaye kukemewa atakufa. 11 Kuzimu na Uharibifu vi wazi mbele za Bwana; Si zaidi basi, mioyo ya wanadamu? 12 Mwenye mzaha hapendi kukaripiwa; Wala yeye hawaendei wenye hekima. 13 Moyo wa furaha huchangamsha uso; Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka. 14 Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa; Bali kinywa cha wapumbavu hula upumbavu. 15 Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya; Bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima. 16 Kuwa na mali chache pamoja na kumcha Bwana; Ni bora kuliko mali nyingi pamoja na taabu. 17 Chakula cha mboga penye mapendano; Ni bora kuliko ng'ombe aliyenona pamoja na kuchukiana. 18 Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano. 19 Njia ya mtu mvivu ni kama boma la miiba; Bali mapito yao wenye unyofu hufanyika njia kuu. 20 Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mpumbavu humdharau mamaye. 21 Upumbavu ni furaha kwake aliyepungukiwa na akili; Bali mwenye ufahamu huunyosha mwenendo wake. 22 Pasipo mashauri makusudi hubatilika; Bali kwa wingi wa washauri huthibithika. 23 Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake; Na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini! 24 Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu; Ili atoke katika kuzimu chini. 25 Bwana ataing'oa nyumba ya mwenye kiburi; Bali atauthibitisha mpaka wa mjane. 26 Mashauri mabaya ni chukizo kwa Bwana; Bali maneno yapendezayo ni safi. 27 Atamaniye faida huifadhaisha nyumba yake mwenyewe; Bali achukiaye zawadi ataishi. 28 Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu; Bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya. 29 Bwana yu mbali na wasio haki; Bali huisikia sala ya mwenye haki. 30 Mng'ao wa macho huufurahisha moyo; Habari njema huinenepesha mifupa. 31 Sikio lisikilizalo lawama yenye uhai Litakaa kati yao wenye hekima. 32 Akataaye maonyo huidharau nafsi yake mwenyewe; Bali yeye asikilizaye lawama hujipatia ufahamu. 33 Kumcha Bwana ni maonyo ya hekima; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu.

Mithali 16

1 Maandalio ya moyo ni ya mwanadamu; Bali jawabu la ulimi hutoka kwa Bwana. 2 Njia zote za mtu ni safi machoni pake mwenyewe; Bali Bwana huzipima roho za watu. 3 Mkabidhi Bwana kazi zako, Na mawazo yako yatathibitika. 4 Bwana amefanya kila kitu kwa kusudi lake; Naam, hata wabaya kwa siku ya ubaya. 5 Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa Bwana; Hakika, hatakosa adhabu. 6 Kwa rehema na kweli uovu husafishwa; Kwa kumcha Bwana watu hujiepusha na maovu. 7 Njia za mtu zikimpendeza Bwana, Hata adui zake huwapatanisha naye. 8 Afadhali mali kidogo pamoja na haki, Kuliko mapato mengi pamoja na udhalimu. 9 Moyo wa mtu huifikiri njia yake; Bali Bwana huziongoza hatua zake. 10 Kukata maneno huwa katika midomo ya mfalme; Kinywa chake hakitakosa katika hukumu. 11 Mizani ya haki na vitanga vyake ni vya Bwana; Mawe yote ya mfukoni ni kazi yake. 12 Wafalme wakitenda yasiyo haki ni chukizo; Maana kiti cha enzi huthibitika kwa haki. 13 Midomo ya haki ni furaha ya wafalme; Nao humpenda yeye asemaye yaliyo sawa. 14 Hasira ya mfalme ni kama wajumbe wa mauti; Lakini mtu mwenye hekima ataituliza. 15 Kuna uhai katika nuru ya uso wa mfalme, Na fadhili zake ni kama wingu la masika. 16 Si afadhali kupata hekima kuliko dhahabu? Naam, yafaa kuchagua ufahamu kuliko fedha. 17 Njia kuu ya mwenye haki ni kujitenga na uovu; Yeye ashikaye njia yake huihifadhi nafsi yake. 18 Kiburi hutangulia uangamivu; Na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko. 19 Afadhali kuwa na roho ya unyenyekevu pamoja na maskini, Kuliko kugawanya nyara pamoja na wenye kiburi. 20 Atakayelitafakari neno atapata mema; Na kila amwaminiye Bwana ana heri. 21 Aliye na hekima moyoni ataitwa mwenye busara; Utamu wa maneno huongeza elimu. 22 Ufahamu ni chemchemi ya uzima kwake aliye nao; Bali kufundishwa kwa wapumbavu ni upuzi wao. 23 Moyo wake mwenye hekima hufundisha kinywa chake; Huzidisha elimu ya midomo yake. 24 Maneno yapendezayo ni kama sega la asali; Ni tamu nafsini, na afya mifupani. 25 Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; Lakini mwisho wake ni njia za mauti. 26 Nafsi yake mfanya kazi hujifanyia kazi; Maana kinywa chake humtia bidii. 27 Mtu asiyefaa kitu huchimba shimo la madhara; Katika midomo yake mna moto uteketezao. 28 Mtu mshupavu huondokesha fitina; Na mchongezi huwafarakanisha rafiki. 29 Mtu mkali humshawishi mwenzake; Humwongoza katika njia isiyo njema. 30 Afumbaye macho, kusudi lake ni kuwaza yaliyopotoka; Aikazaye midomo yake hutokeza mabaya. 31 Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, Kama kikionekana katika njia ya haki. 32 Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; Na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji. 33 Kura hutupwa katika mikunjo ya nguo; Lakini hukumu zake zote ni za Bwana.

Mithali 17

1 Afadhali mego kavu pamoja na utulivu, Kuliko nyumba yenye karamu nyingi pamoja na magomvi. 2 Mtumwa atendaye kwa busara atamtawala mwana atendaye mambo ya aibu; Tena atapata sehemu ya urithi kati ya ndugu. 3 Kalibuni kwa fedha, na tanuru kwa dhahabu; Bali Bwana huijaribu mioyo. 4 Mtenda mabaya husikiliza midomo ya uovu; Na mwongo hutega sikio lake kusikiliza ulimi wa madhara. 5 Amdhihakiye maskini humsuta Muumba wake; Naye aufurahiaye msiba hatakosa adhabu. 6 Wana wa wana ndio taji ya wazee, Na utukufu wa watoto ni baba zao. 7 Maneno mazuri hayapendezi kinywani mwa mpumbavu; Siuze midomo ya uongo kinywani mwa mkuu. 8 Kipawa ni kama kito cha thamani machoni pake yeye aliye nacho; Kila kigeukapo hufanikiwa. 9 Afunikaye kosa hutafuta kupendwa; Bali yeye akashifuye neno hutenga rafiki. 10 Lawama hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu, Kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu. 11 Mtu mwovu hataki neno ila kuasi tu; Kwa hiyo mjumbe mkali atatumwa kwake. 12 Afadhali mtu akutwe na dubu aliyenyang'anywa watoto wake, Kuliko na mpumbavu katika upumbavu wake. 13 Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, Mabaya hayataondoka nyumbani mwake. 14 Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; Basi acheni ugomvi kabla haujafurika. 15 Yeye asemaye kwamba asiye haki ana haki; naye asemaye kwamba mwenye haki hana haki; Hao wote wawili ni chukizo kwa Bwana. 16 Nini maana yake, mpumbavu kuwa na fedha mkononi mwake ya kununulia hekima, Ikiwa hana moyo wa ufahamu? 17 Rafiki hupenda sikuzote; Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu. 18 Aliyepungukiwa na akili hupana mkono na mtu; Na kuwa mdhamini mbele ya mwenzake. 19 Apendaye ugomvi hupenda dhambi; Auinuaye sana mlango wake hutafuta uharibifu. 20 Mtu mwenye moyo wa ukaidi hatapata mema; Na mwenye ulimi wa upotofu huanguka katika misiba. 21 Azaaye mpumbavu ni kwa huzuni yake mwenyewe; Wala baba wa mpumbavu hana furaha. 22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; Bali roho iliyopondeka huikausha mifupa. 23 Asiye haki hutoa rushwa kifuani, Ili kuzipotosha njia za hukumu. 24 Hekima huwa machoni pake mwenye ufahamu; Bali macho ya mpumbavu huwa katika ncha za dunia. 25 Mwana mpumbavu ni huzuni kwa babaye, Na uchungu kwa mamaye aliyemzaa. 26 Tena kumwadhibu mwenye haki si vizuri; Wala si kwema kuwapiga wakuu kwa unyofu wao. 27 Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; Na mwenye roho ya utulivu ana busara. 28 Hata mpumbavu akinyamaza, huhesabiwa hekima; Akifumba midomo yake, huhesabiwa ufahamu.

Mithali 18

1 Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; Hushindana na kila shauri jema. 2 Mpumbavu hapendezwi na ufahamu; Ila moyo wake udhihirike tu. 3 Ajapo asiye haki, huja dharau pia; Na pamoja na aibu huja lawama. 4 Maneno ya kinywa cha mtu ni kama maji ya vilindi; Kijito kibubujikacho; chemchemi ya hekima. 5 Kukubali uso wake asiye haki si vizuri; Wala kumpotosha mwenye haki hukumuni. 6 Midomo ya mpumbavu huingia katika fitina, Na kinywa chake huita mapigo. 7 Kinywa cha mpumbavu ni uharibifu wake, Na midomo yake ni mtego wa nafsi yake. 8 Maneno ya mchongezi ni kama vitoweo; Nayo hushukia pande za ndani za tumbo. 9 Yeye naye aliye mvivu katika kazi yake, Ni ndugu yake aliye mharabu. 10 Jina la Bwana ni ngome imara; Mwenye haki huikimbilia, akawa salama. 11 Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; Ni kama ukuta mrefu katika mawazo yake. 12 Kabla ya uharibifu moyo wa mwanadamu hujivuna; Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu. 13 Yeye ajibuye kabla hajasikia, Ni upumbavu na aibu kwake. 14 Roho ya mtu itastahimili udhaifu wake; Bali roho iliyovunjika nani awezaye kuistahimili? 15 Moyo wa mwenye busara hupata maarifa; Na sikio la mwenye hekima hutafuta maarifa. 16 Zawadi ya mtu humpatia nafasi; Humleta mbele ya watu wakuu. 17 Ajiteteaye kwanza huonekana kuwa ana haki; Lakini jirani yake huja na kumchunguza. 18 Kura hukomesha mashindano; Hukata maneno ya wakuu. 19 Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu; Na mashindano ni kama mapingo ya ngome. 20 Tumbo la mtu litajazwa matunda ya kinywa chake; Atashiba mazao ya midomo yake. 21 Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake. 22 Apataye mke apata kitu chema; Naye ajipatia kibali kwa Bwana. 23 Maskini hutumia maombi; Bali tajiri hujibu kwa ukali. 24 Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe; Lakini yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.

Mithali 19

1 Afadhali maskini aendaye katika unyofu wake, Kuliko mpotofu wa midomo aliye mpumbavu. 2 Tena si vizuri nafsi ya mtu ikose maarifa; Naye afanyaye haraka kwa miguu hutenda dhambi. 3 Upumbavu wa mtu hupotosha njia yake; Na moyo wake hununa juu ya Bwana. 4 Utajiri huongeza rafiki wengi; Bali maskini hutengwa na rafiki yake. 5 Shahidi wa uongo hakosi ataadhibiwa; Wala asemaye uongo hataokoka. 6 Watu wengi watamsihi mkuu ili awafadhili; Na kila mtu ni rafiki yake atoaye tunu. 7 Ndugu zote wa maskini humchukia; Jinsi gani rafiki zake huzidi kujitenga naye! Huwafuata kwa maneno, lakini wametoweka. 8 Apataye hekima hujipenda nafsi yake; Ashikaye ufahamu atapata mema. 9 Shahidi wa uongo hakosi ataadhibiwa; Naye asemaye uongo ataangamia. 10 Maisha ya anasa hayampasi mpumbavu; Sembuse mtumwa awatawale wakuu. 11 Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; Nayo ni fahari yake kusamehe makosa. 12 Ghadhabu ya mfalme ni kama ngurumo ya simba; Bali hisani yake kama umande juu ya majani. 13 Mwana mpumbavu ni msiba kwa babaye; Na ugomvi wa mke kama kutona-tona daima. 14 Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye; Bali mke mwenye busara, mtu hupewa na Bwana. 15 Uvivu humtia mtu katika usingizi mzito; Na nafsi yake mvivu itaona njaa. 16 Yeye aihifadhiye amri huihifadhi nafsi yake; Bali yeye asiyeziangalia njia zake atakufa. 17 Amhurumiaye maskini humkopesha Bwana; Naye atamlipa kwa tendo lake jema. 18 Mrudi mwanao, kwa maana liko tumaini; Wala usiikaze nafsi yako kwa kuangamia kwake. 19 Mtu wa hasira nyingi atachukua adhabu yake, Maana ujapomwokoa huna budi kufanya tena. 20 Sikiliza mashauri, ukapokee mafundisho, Upate kuwa na hekima siku zako za mwisho. 21 Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; Lakini shauri la Bwana ndilo litakalosimama. 22 Haja ya mwanadamu ni hisani yake; Ni afadhali maskini kuliko mwongo. 23 Kumcha Bwana huelekea uhai; Atakaa ameshiba; hatajiliwa na ubaya. 24 Mtu mvivu hutia mkono wake sahanini; Ila hataki hata kuupeleka kinywani pake. 25 Mpige mwenye mzaha, na mjinga atapata busara; Mwonye mwenye ufahamu, naye atatambua maarifa. 26 Apotezaye mali za babaye na kumfukuza mamaye, Ni mwana aaibishaye, na kuleta lawama. 27 Mwanangu, acha kusikia mafundisho, Ukitaka tu kuyaasi maneno ya maarifa. 28 Shahidi asiyefaa kitu hudhihaki hukumu, Na vinywa vya wasio haki humeza uovu. 29 Hukumu zimewekwa tayari kwa wenye mzaha; Na mapigo kwa mgongo wa wapumbavu.

Mithali 20

1 Mvinyo hudhihaki, kileo huleta ugomvi; Na akosaye kwa vitu hivyo hana hekima. 2 Utisho wa mfalme ni kama ngurumo ya simba; Amkasirishaye huitendea dhambi nafsi yake. 3 Mtu kujitenga na ugomvi ni heshima kwake; Bali kila mpumbavu ataka kugombana. 4 Mtu mvivu hataki kulima wakati wa baridi; Hivyo wakati wa mavuno ataomba, hana kitu. 5 Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; Lakini mtu mwenye ufahamu atayateka. 6 Wanadamu hutangaza kila mtu hisani yake mwenyewe; Bali mtu aliye mwaminifu, ni nani awezaye kumpata? 7 Mwenye haki aendaye katika unyofu wake, Watoto wake wabarikiwa baada yake. 8 Mfalme aketiye katika kiti cha hukumu, Huyapepeta mabaya yote kwa macho yake. 9 Nani awezaye kusema, Nimesafisha moyo wangu; Nimetakasika dhambi yangu? 10 Vipimo mbalimbali, na pishi mbalimbali, Vyote viwili ni chukizo kwa Bwana. 11 Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; Kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili. 12 Sikio lisikialo, na jicho lionalo, Bwana ndiye aliyeyafanya yote mawili. 13 Usipende usingizi usije ukawa maskini; Fumbua macho yako nawe utashiba chakula. 14 Haifai kitu, haifai kitu, asema mnunuzi; Lakini akiisha kwenda zake hujisifu. 15 Dhahabu iko, na marijani tele; Lakini midomo ya maarifa ni kito cha thamani. 16 Twaa nguo yake amdhaminiye mgeni; Mtoze rehani aliye mdhamini wa wageni. 17 Chakula cha uongo ni kitamu kwa mtu; Lakini halafu kinywa chake kitajaa changarawe. 18 Kila kusudi huthibitika kwa kushauriana; Na kwa shauri la akili fanya vita. 19 Mwenye kitango akisingizia hufunua siri; Basi, usishirikiane naye afunuaye midomo yake sana. 20 Amlaaniye babaye au mamaye, Taa yake itazimika katika giza kuu. 21 Urithi uliopatikana mwanzo kwa haraka, Mwisho wake, lakini, hautabarikiwa. 22 Usiseme, Mimi nitalipa mabaya; Mngojee Bwana, naye atakuokoa. 23 Vipimo mbalimbali ni chukizo kwa Bwana; Tena mizani ya hila si njema. 24 Mwenendo wa mtu watoka kwa Bwana; Basi, awezaje mtu kuelewa na njia yake? 25 Ni mtego, mtu aseme kwa haraka, Kitu hiki ni wakfu; Na baada ya kuweka nadhiri kuuliza-uliza habari. 26 Mfalme mwenye hekima huwapepeta wasio haki; Naye hulipitisha gurudumo la kupuria juu yao. 27 Pumzi ya mwanadamu ni taa ya Bwana; Hupeleleza yote yaliyomo ndani yake. 28 Fadhili na uaminifu humhifadhi mfalme, Na kiti chake cha enzi huthibitishwa kwa fadhili. 29 Fahari ya vijana ni nguvu zao, Na uzuri wa wazee ni kichwa chenye mvi. 30 Machubuko ya fimbo husafisha uovu, Na mapigo hufikilia ndani ya mtima.

Mithali 21

1 Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa Bwana; Kama mifereji ya maji huugeuza po pote apendapo. 2 Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe; Bali Bwana huipima mioyo. 3 Kutenda haki na hukumu Humpendeza Bwana kuliko kutoa sadaka. 4 Macho yenye kiburi, na moyo wa kutakabari, Hata ukulima wa waovu, ni dhambi. 5 Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu; Bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji. 6 Kupata akiba ya mali kwa ulimi wa uongo Ni moshi upeperushwao; ni kutafuta mauti. 7 Jeuri ya wabaya itawaondolea mbali; Kwa sababu wamekataa kutenda hukumu. 8 Njia yake aliyelemewa na dhambi imepotoka sana; Bali mtu aliye safi, kazi yake ni sawasawa. 9 Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini, Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi. 10 Nafsi ya mtu mbaya hutamani uovu; Jirani yake hapati fadhili machoni pake. 11 Mwenye mzaha aadhibiwapo, mjinga hupata hekima; Na mwenye hekima afundishwapo, hupokea maarifa. 12 Mwenye haki huitafakari nyumba ya mtu mbaya; Jinsi wabaya waangushwavyo wakaangamia. 13 Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini, Yeye naye atalia, lakini hatasikiwa. 14 Kipawa cha siri hutuliza hasira; Na rushwa bindoni humliza ghadhabu kali. 15 Ni furaha yao wenye haki kutenda hukumu; Lakini ni uharibifu kwao watendao maovu. 16 Mtu aikosaye njia ya busara Atakaa katika mkutano wao waliokufa. 17 Mtu apendaye anasa atakuwa maskini; Apendaye mvinyo na mafuta hatakuwa tajiri. 18 Mtu asiye haki ni fidia ya wenye haki; Naye afanyaye hila ni badala ya watu wa adili. 19 Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika; Kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi. 20 Kuna hazina ya thamani na mafuta katika maskani ya mwenye hekima; Bali mwanadamu aliye mpumbavu huyameza. 21 Aandamaye haki na fadhili, Ataona uhai na haki na heshima. 22 Mwenye hekima huupandia mji wao wenye nguvu; Na kuziangusha nguvu za tumaini lao. 23 Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake, Atajilinda nafsi yake na taabu. 24 Mwenye kiburi na kutakabari, jina lake ni mbishi; Hutenda mambo katika majivuno ya kiburi chake. 25 Matakwa yake mtu mvivu humfisha, Kwa maana mikono yake hukataa kufanya kazi. 26 Kuna atamaniye kwa choyo mchana kutwa; Bali mwenye haki hutoa wala hanyimi. 27 Sadaka ya wasio haki ni chukizo; Si zaidi sana ailetapo mwenye nia mbaya! 28 Shahidi wa uongo atapotea; Bali mtu asikiaye atasema maneno yadumuyo. 29 Asiye haki huufanya uso wake kuwa mgumu; Bali mtu mnyofu huzifikiri njia zake. 30 Hapana hekima, wala ufahamu, Wala shauri, juu ya Bwana. 31 Farasi huwekwa tayari kwa siku ya vita; Lakini Bwana ndiye aletaye wokovu.

Mithali 22

1 Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; Na neema kuliko fedha na dhahabu. 2 Tajiri na maskini hukutana pamoja; Bwana ndiye aliyewaumba wote wawili. 3 Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; Bali wajinga huendelea mbele wakaumia. 4 Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha Bwana Ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima. 5 Miiba na mitego huwa katika njia ya mshupavu; Yeye aitunzaye nafsi yake atakuwa mbali nayo. 6 Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee. 7 Tajiri humtawala maskini, Naye akopaye ni mtumwa wake akopeshaye. 8 Yeye apandaye uovu atavuna msiba, Na fimbo ya ghadhabu yake itakoma. 9 Mwenye jicho la ukarimu atabarikiwa; Maana huwapa maskini chakula chake. 10 Mtupe nje mwenye dharau, na ugomvi utatoka; Naam, fitina na fedheha zitakoma. 11 Apendaye usafi wa moyo, na neema ya midomo; Mfalme atakuwa rafiki yake. 12 Macho ya Bwana humhifadhi mwenye maarifa; Bali huyapindua maneno ya mtu haini. 13 Mtu mvivu husema, Simba yuko nje; Nitauawa katika njia kuu. 14 Kinywa cha malaya ni shimo refu; Anayechukiwa na Bwana atatumbukia ndani yake. 15 Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali. 16 Yeye awaoneaye maskini ili kuongeza mapato, Naye ampaye tajiri, hupata hasara. 17 Tega sikio lako uyasikie maneno ya wenye hekima, na kuuelekeza moyo wako kwa maarifa yangu; 18 maana ni vizuri kuyahifadhi ndani yako, hali yakithibitika pamoja midomoni mwako. 19 Ili matumaini yako uyaweke kwa Bwana, leo nimekujulisha wewe haya, naam, wewe. 20 Je! Sikukuandikia mambo makuu juu ya mashauri na juu ya maarifa; 21 ili kukujulisha hakika ya maneno ya kweli, uwarudishie wakutumao maneno ya kweli? 22 Usimnyang'anye maskini, kwa kuwa ni maskini; Wala usimdhulumu mtu mnyonge langoni; 23 Kwa sababu Bwana atawatetea; Naye atawateka uhai wao waliowateka. 24 Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi; Wala usiende na mtu wa ghadhabu nyingi; 25 Usije ukajifunza njia zake; Na kujipatia nafsi yako mtego. 26 Usiwe mmoja wao wawekao rehani; Au walio wadhamini kwa deni za watu; 27 Kama huna kitu cha kulipa; Kwani ukaondolee kitanda chako chini yako? 28 Usiiondoe alama ya mpaka wa zamani, Uliowekwa na baba zako. 29 Je! Wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme; Hatasimama mbele ya watu wasio na cheo.

Mithali 23

1 Utakapoketi kwa chakula pamoja na mtawala, Mwangalie sana yeye aliye mbele yako. 2 Tena ujitie kisu kooni, Kama ukiwa mlafi. 3 Usivitamani vyakula vyake vya anasa; Kwa maana ni vyakula vya hila. 4 Usijitaabishe ili kupata utajiri; Acha kuzitegemea akili zako mwenyewe. 5 Je! Utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, Kama tai arukaye mbinguni. 6 Usile mkate wa mtu mwenye husuda; Wala usivitamani vyakula vyake vya anasa; 7 Maana aonavyo nafsini mwake, ndivyo alivyo. Akuambia, Haya, kula, kunywa; Lakini moyo wake hauwi pamoja nawe. 8 Tonge lile ulilokula utalitapika, Na maneno yako matamu yatakupotea. 9 Usiseme masikioni mwa mpumbavu; Maana atadharau hekima ya maneno yako. 10 Usiiondoe alama ya mpaka wa zamani; Wala usiingie katika mashamba ya yatima; 11 Kwa sababu mkombozi wao ana nguvu; Atawatetea juu yako. 12 Elekeza moyo wako kusikiliza mafundisho; Tega masikio yako kusikia maneno ya maarifa. 13 Usimnyime mtoto wako mapigo; Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. 14 Utampiga kwa fimbo, Na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu. 15 Mwanangu, kama moyo wako una hekima, Moyo wangu utafurahi, naam, moyo wangu; 16 Naam, viuno vyangu vitafurahi, Midomo yako inenapo maneno mema. 17 Moyo wako usiwahusudu wenye dhambi; Bali mche Bwana mchana kutwa; 18 Maana bila shaka iko thawabu; Na tumaini lako halitabatilika. 19 Sikia, mwanangu, uwe na hekima, Na kuuongoza moyo wako katika njia njema. 20 Usiwe miongoni mwao wanywao mvinyo; Miongoni mwao walao nyama kwa pupa. 21 Kwa maana mlevi na mlafi huingia umaskini, Na utepetevu humvika mtu nguo mbovu. 22 Msikilize baba yako aliyekuzaa, Wala usimdharau mama yako akiwa mzee. 23 Inunue kweli, wala usiiuze; Naam, hekima, na mafundisho, na ufahamu. 24 Baba yake mwenye haki atashangilia; Naye amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia. 25 Na wafurahi baba yako na mama yako; Na afurahi aliyekuzaa. 26 Mwanangu, nipe moyo wako; Macho yako yapendezwe na njia zangu. 27 Kwa maana kahaba ni shimo refu; Na malaya ni rima jembamba. 28 Naam, huotea kama mnyang'anyi; Huwaongeza wenye hila katika wanadamu. 29 Ni nani apigaye, Yowe? Ni nani aliaye, Ole? Ni nani mwenye ugomvi? Ni nani mwenye mguno? Ni nani aliye na jeraha zisizo na sababu? Ni nani aliye na macho mekundu? 30 Ni wale wakaao sana kwenye mvinyo; Waendao kutafuta divai iliyochanganyika. 31 Usiitazame mvinyo iwapo ni nyekundu; Iitiapo bilauri rangi yake, ishukapo taratibu; 32 Mwisho wake huuma kama nyoka; Huchoma kama fira. 33 Macho yako yataona mambo mageni; Na moyo wako utatoa yaliyopotoka. 34 Naam, utakuwa kama alalaye katikati ya bahari; Au kama yeye asinziaye juu ya mlingoti. 35 Utasema, Wamenichapa wala sikuumia; Wamenipiga wala sina habari; Nitaamka lini, nitazidi kuitafuta tena.

Mithali 24

1 Usiwahusudu watu waovu, Wala usitamani kuwa pamoja nao; 2 Kwa maana moyo wao hufikiri dhuluma, Na midomo yao huongea madhara. 3 Nyumba hujengwa kwa hekima, Na kwa ufahamu huthibitika, 4 Na kwa maarifa vyumba vyake hujazwa Vitu vyote vya thamani na vya kupendeza. 5 Mtu mwenye hekima ana nguvu; Naam, mtu wa maarifa huongeza uwezo; 6 Maana kwa mashauri ya akili utafanya vita; Na kwa wingi wa washauri huja wokovu. 7 Kwa mpumbavu hekima haipatikani; Hafumbui kinywa chake langoni. 8 Mtu afikiriye kutenda maovu, Watu watamwita mtundu; 9 Fikira za mpumbavu ni dhambi, Na mwenye mzaha huwachukiza watu. 10 Ukizimia siku ya taabu, Nguvu zako ni chache. 11 Uwaokoe wanaochukuliwa ili wauawe; Nao walio tayari kuchinjwa uwaopoe. 12 Ukisema, Sisi hatukujua hayo; Je! Yeye aipimaye mioyo siye afahamuye? Naye ailindaye nafsi yako siye ajuaye? Je! Hatamlipa kila mtu sawasawa na kazi yake? 13 Mwanangu, ule asali, kwa maana ni njema, Na sega la asali lililo tamu ulionjapo. 14 Basi utaijua hekima kuwa tamu kwa nafsi yako; Ikiwa umekwisha kuiona; Ndipo itakapofuata thawabu; Wala tumaini lako halitabatilika. 15 Ewe mtu mbaya, usiyavizie makao yake mwenye haki; Wala usipaharibu mahali pake pa kupumzika; 16 Kwa maana mwenye haki huanguka mara saba akaondoka tena; Bali wasio haki hukwazwa na mabaya. 17 Usifurahi, adui yako aangukapo; Wala moyo wako usishangilie ajikwaapo; 18 Bwana asije akaliona hilo, likamkasirisha; Akageuzia mbali naye hasira yake. 19 Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya; Wala usiwahusudu wabaya; 20 Kwa maana mtu mbaya hapati thawabu; Taa ya mtu mbaya itazimika. 21 Mwanangu, mche Bwana, na mfalme; Wala usishirikiane na wenye kigeugeu; 22 Maana msiba wao utatokea kwa ghafula; Tena ni nani aujuaye uharibifu wa miaka yao. 23 Haya nayo pia ni maneno ya wenye akili. Kupendelea watu katika hukumu si kwema. 24 Amwambiaye mtu mwovu, Wewe una haki; Kabila za watu watamlaani, taifa watamchukia. 25 Bali kwao wakemeao furaha itakuwako; Na baraka ya kufanikiwa itawajilia. 26 Aibusu midomo atoaye jawabu la haki. 27 Tengeneza kazi yako huko nje, Jifanyizie kazi yako tayari shambani, Ukiisha, jenga nyumba yako. 28 Usimshuhudie jirani yako pasipo sababu, Wala usidanganye kwa midomo yako. 29 Usiseme, Nitamtenda kama alivyonitenda mimi; Nitamlipa mtu huyo sawasawa na tendo lake. 30 Nalipita karibu na shamba la mvivu, Na shamba la mizabibu la mtu asiye na akili. 31 Kumbe! Lote pia limemea miiba; Uso wake ulifunikwa kwa viwawi; Na ukuta wake wa mawe umebomoka. 32 Ndipo nilipoangalia na kufikiri sana; Naliona, nikapata mafundisho. 33 Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, Bado kukunja mikono upate usingizi! 34 Hivyo, umaskini wako huja kama mnyang'anyi, Na uhitaji wako kama mtu mwenye silaha.

Mithali 25

1 Hizi nazo ni mithali za Sulemani, ambazo watu wa Hezekia, mfalme wa Yuda, walizinakili. 2 Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo; Bali ni utukufu wa mfalme kuchunguza jambo. 3 Mbingu huenda juu sana, na nchi huenda chini; Lakini mioyo ya wafalme haichunguziki. 4 Ondoa takataka katika fedha, Na chombo kitatokea kwa mtakasaji; 5 Mwondoe asiye haki mbele ya mfalme, Na kiti chake cha enzi kitathibitika katika haki. 6 Usijitukuze mbele ya uso wa mfalme; Wala usisimame mahali pa watu wakuu; 7 Kwa maana ni heri kuambiwa, Njoo huku mbele; Kuliko kuwekwa nyuma machoni pa mkuu. Yale uliyoyaona kwa macho, 8 Usitoke nje kwa haraka ili kuyashindania; Usije ukakosa kujua la kutenda hatimaye, Mwenzako atakapokuwa amekuaibisha. 9 Ujitetee na mwenzako peke yake; Bali usiifunue siri ya mtu mwingine; 10 Yeye asikiaye asije akakutukana; Na aibu yako isiondoke. 11 Neno linenwalo wakati wa kufaa, Ni kama machungwa katika vyano vya fedha. 12 Kipuli cha dhahabu, na pambo la dhahabu safi; Ndivyo alivyo mwonyaji mwenye hekima kwa sikio lisikialo. 13 Kama baridi ya theluji wakati wa mavuno; Ndivyo alivyo mjumbe mwaminifu kwao wamtumao; Kwa maana huwaburudisha bwana zake nafsi zao. 14 Kama mawingu na upepo pasipo mvua; Ndivyo alivyo yeye ajisifiaye karama kwa uongo. 15 Kwa uvumilivu mwingi mkuu husadikishwa; Na ulimi laini huvunja mfupa. 16 Je! Umeona asali? Kula kadiri ya kukutosha; Usije ukashiba na kuitapika. 17 Mguu wako usiingie katika nyumba ya jirani yako ila kwa kiasi; Asije akakukinai na kukuchukia. 18 Mtu amshuhudiaye jirani yake uongo Ni nyundo, na upanga, na mshale mkali. 19 Kumtumaini asiye mwaminifu wakati wa taabu Ni kama jino lililovunjika, au mguu ulioteguka. 20 Amwimbiaye nyimbo mtu mwenye moyo mzito, Ni kama yeye avuaye nguo wakati wa baridi; Ni kama siki juu ya magadi. 21 Adui yako akiwa ana njaa, mpe chakula; Tena akiwa ana kiu, mpe maji ya kunywa; 22 Maana utatia makaa ya moto kichwani pake; Na Bwana atakupa thawabu. 23 Upepo wa kusi huleta mvua; Vile vile asingiziaye huleta uso wa ghadhabu. 24 Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini, Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi. 25 Kama vile maji ya baridi kwa mtu mwenye kiu, Ndivyo ilivyo habari njema itokayo katika nchi ya mbali. 26 Mwenye haki amwangukiapo mtu mbaya Ni kama chemchemi iliyochafuka, Na kisima kilichokanyagwa. 27 Haifai kula asali nyingi mno; Vile vile mtu kutafuta utukufu wake mwenyewe si utukufu. 28 Asiyetawala roho yake Ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.

Mithali 26

1 Kama theluji wakati wa joto, na mvua wakati wa mavuno; Kadhalika heshima haimpasi mpumbavu. 2 Kama shomoro katika kutanga-tanga kwake, Na kama mbayuwayu katika kuruka kwake; Kadhalika laana isiyo na sababu haimpigi mtu. 3 Mjeledi kwa farasi, lijamu kwa punda, Na fimbo kwa mgongo wa mpumbavu. 4 Usimjibu mpumbavu sawasawa na upumbavu wake; Usije ukafanana naye. 5 Umjibu mpumbavu sawasawa na upumbavu wake; Asije akawa mwenye hekima machoni pake. 6 Apelekaye ujumbe kwa mkono wa mpumbavu Hujikata miguu, na kunywa hasara. 7 Miguu yake achechemeaye huwa dhaifu; Kadhalika mithali katika kinywa cha mpumbavu. 8 Kama mfuko wa vito katika chungu ya mawe; Kadhalika mtu amheshimuye mpumbavu. 9 Kama mwiba uingiao katika mkono wa mlevi; Kadhalika mithali katika kinywa cha mpumbavu. 10 Fundi stadi hufanyiza vitu vyote; Bali amwajiriye mpumbavu ni kama awaajiriye watu wapitao. 11 Kama vile mbwa arudiavyo matapiko yake; Kadhalika mpumbavu afanya upumbavu tena. 12 Je! Wamwona mtu mwenye hekima machoni pake mwenyewe? Afadhali kumtumaini mpumbavu kuliko yeye. 13 Mtu mvivu husema, Simba yuko njiani, Simba yuko katika njia kuu. 14 Kama vile mlango ugeukavyo katika bawaba zake; Kadhalika mtu mvivu katika kitanda chake. 15 Mtu mvivu hutia mkono wake sahanini; Kwamchosha kuupeleka tena kinywani pake. 16 Mtu mvivu ni mwenye hekima machoni pake, Kuliko watu saba wawezao kutoa sababu. 17 Mtu apitaye na kujisumbua kwa ugomvi usio wake; Ni kama mtu ashikaye mbwa kwa masikio yake. 18 Kama mtu mwenye wazimu atupaye mienge, Na mishale, na mauti; 19 Ndivyo alivyo amdanganyaye mwenzake, Na kusema, Je! Sikufanya mzaha tu? 20 Moto hufa kwa kukosa kuni; Na bila mchongezi fitina hukoma. 21 Kama makaa juu ya makaa yanayowaka, Na kama kuni juu ya moto; Ndivyo mtu mgomvi achocheavyo uadui. 22 Maneno ya mchongezi ni kama vitoweo. Nayo hushukia pande za ndani za tumbo. 23 Midomo ijipendekezayo pamoja na moyo mbaya Ni kama kigae kilichofunikizwa taka za fedha. 24 Achukiaye huficha chuki kwa midomo yake; Naye huweka akiba ya hila moyoni mwake. 25 Anenapo maneno mazuri usimsadiki; Kwa maana ana machukizo saba moyoni mwake. 26 Ingawa chuki hufunikizwa kwa hila; Uovu wake utadhihirika mbele ya kusanyiko. 27 Achimbaye shimo atatumbukia mwenyewe; Naye abingirishaye jiwe litamrudia. 28 Ulimi unenao uongo huwachukia wale uliowajeruhi; Na kinywa cha kujipendekeza hutenda uharibifu.

Mithali 27

1 Usijisifu kwa ajili ya kesho; Kwa maana hujui yatakayozaliwa na siku moja. 2 Mwingine na akusifu wala si kinywa chako mwenyewe; Mtu mgeni wala si midomo yako wewe. 3 Jiwe ni zito, na mchanga hulemea; Lakini ghadhabu ya mpumbavu ni nzito kuliko hivi vyote viwili. 4 Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; Lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya wivu. 5 Lawama ya wazi ni heri, Kuliko upendo uliositirika. 6 Jeraha utiwazo na rafiki ni amini; Bali kubusu kwa adui ni kwingi sana. 7 Nafsi iliyoshiba hukinai sega la asali; Bali nafsi yenye njaa huona kila kitu kichungu kuwa kitamu. 8 Kama ndege aendaye huko na huko mbali na kitundu chake; Ndivyo alivyo mtu aendaye huko na huko mbali na mahali pake. 9 Marhamu na manukato huufurahisha moyo; Kadhalika utamu wa rafiki ya mtu utokao katika kusudi la moyo wake. 10 Usimwache rafiki yako mwenyewe, wala rafiki ya baba yako, Wala usiende nyumbani mwa ndugu yako siku ya msiba wako. Afadhali jirani aliye karibu kuliko ndugu aliye mbali. 11 Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; Ili nipate kumjibu anilaumuye. 12 Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; Bali wajinga huendelea mbele wakaumia. 13 Twaa nguo yake amdhaminiye mgeni; Mtoza rehani aliye mdhamini wa malaya. 14 Mtu ambarikiye mwenzake kwa sauti kuu asubuhi na mapema; Itahesabiwa kuwa ni laana kwake. 15 Kutona-tona daima siku ya mvua nyingi, Na mwanamke mgomvi ni sawasawa; 16 Atakaye kumzuia huyo huuzuia upepo; Na mkono wake wa kuume hukuta mafuta. 17 Chuma hunoa chuma; Ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake. 18 Yeye autunzaye mtini atakula matunda yake; Naye amhudumiaye bwana wake ataheshimiwa. 19 Kama uso ufananavyo na uso katika maji; Kadhalika moyo wa mtu na mwenzake. 20 Kuzimu na Uharibifu havishibi; Wala macho ya wanadamu hayashibi. 21 Kalibu ni kwa fedha, na tanuru kwa dhahabu; Na mtu hujaribiwa kwa sifa zake. 22 Hata ukimtwanga mpumbavu kwa mchi kinuni pamoja na ngano; Upumbavu wake hautamtoka. 23 Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako; Na kuwaangalia sana ng'ombe zako. 24 Kwa maana mali haziwi za milele; Na taji je! Yadumu tangu kizazi hata kizazi? 25 Manyasi huchukuliwa, na majani mabichi huonekana, Na maboga ya milimani hukusanyika. 26 Wana-kondoo hufaa kwa mavazi yako; Na mbuzi ni thamani ya shamba 27 Tena yatakuwapo maziwa ya mbuzi, Ya kukutosha kwa chakula chako, Na chakula cha watu wa nyumbani mwako, Na posho la vijakazi vyako.

Mithali 28

1 Waovu hukimbia wasipofuatiwa na mtu; Bali wenye haki ni wajasiri kama simba. 2 Kwa sababu ya maasi ya nchi wakuu wake huwa wengi; Bali kwa wenye ufahamu na maarifa hali ya nchi hudumishwa 3 Mtu mhitaji awaoneaye maskini, Ni kama mvua ya dhoruba isiyosaza chakula. 4 Wao waiachao sheria huwasifu waovu; Bali wao waishikao hushindana nao. 5 Watu wabaya hawaelewi na hukumu; Bali wamtafutao Bwana huelewa na yote. 6 Afadhali maskini aendaye katika unyofu wake, Kuliko mpotofu wa njia angawa ni tajiri. 7 Yeye aishikaye sheria ni mwana mwenye hekima; Bali aliye rafiki wa walafi humwaibisha babaye. 8 Yeye azidishaye mali yake kwa riba na faida, Humkusanyia mtu awahurumiaye maskini. 9 Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, Hata sala yake ni chukizo. 10 Kila mtu awapotezaye wenye haki katika njia mbaya, Ataanguka katika rima lake mwenyewe; Bali wakamilifu watarithi mema. 11 Mtu tajiri ana hekima machoni pake mwenyewe; Bali maskini mwenye ufahamu humchunguza sana. 12 Wenye haki washindapo, uko utukufu mwingi; Bali waovu waondokapo, watu hujificha. 13 Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema. 14 Mwanadamu mwenye kicho yu heri sikuzote; Bali mshupavu wa moyo ataangukia madhara. 15 Kama simba angurumaye, na dubu mwenye njaa; Ndivyo alivyo mtu mbaya awatawalaye maskini. 16 Mkuu aliyepungukiwa na akili huwaonea watu sana; Bali achukiaye kutamani ataongeza siku zake. 17 Aliyelemewa na damu ya mtu Atalikimbilia shimo; wala mtu asimzuie. 18 Aendaye kwa unyofu ataokolewa; Bali mkaidi wa njia zake ataanguka mara. 19 Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele; Bali afuataye mambo ya upuzi atapata umaskini wa kumtosha. 20 Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; Lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa. 21 Kupendelea watu si kwema; Wala mtu kuasi kwa ajili ya kipande cha mkate. 22 Mwenye husuda afanya haraka kuwa tajiri; Wala haufikiri uhitaji utakaomjilia. 23 Amkemeaye mwenzake hatimaye atapata kibali; Zaidi ya mtu ajipendekezaye kwa ulimi wake. 24 Aibaye mali ya babaye au mamaye, na kusema, Si kosa; Mwana huyo ni rafiki wa mtu mharibifu. 25 Mwenye nafsi ya kutamani huchochea fitina; Bali amtumainiye Bwana atawandishwa. 26 Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga; Bali yeye aendaye kwa busara ataokolewa. 27 Mwenye kuwagawia maskini hatahitaji kitu; Bali afichaye macho yake atakuwa na laana nyingi. 28 Wasio haki wainukapo, wanadamu hujificha; Bali waangamiapo, wenye haki huongezeka.

Mithali 29

1 Aonywaye mara nyingi akishupaza shingo, Atavunjika ghafula, wala hapati dawa. 2 Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi; Bali mwovu atawalapo, watu huugua. 3 Apendaye hekima humfurahisha babaye; Bali ashikamanaye na makahaba hutapanya mali. 4 Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua. 5 Mwenye kujipendekeza kwa jirani yake, Hutandika wavu ili kuitega miguu yake. 6 Kuna mtego katika kosa la mtu mbaya; Bali mwenye haki huimba na kufurahi. 7 Mwenye haki huyaangalia madai ya maskini; Bali mtu mbaya hana ufahamu hata ayajue. 8 Watu wenye dharau huwasha mji moto; Bali wenye hekima hugeuzia mbali ghadhabu. 9 Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha. 10 Wamwagao damu humchukia mtu mkamilifu; Bali wenye haki humtunza nafsi yake. 11 Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; Bali mwenye hekima huizuia na kuituliza. 12 Mwenye kutawala akisikiliza uongo; Basi watumishi wake wote watakuwa waovu. 13 Maskini na mdhalimu hukutana pamoja; Bwana huwatia nuru macho yao wote wawili. 14 Mfalme awahukumuye maskini kwa uaminifu; Kiti chake cha enzi kitathibitika milele. 15 Fimbo na maonyo hutia hekima; Bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye. 16 Waovu wakiongezeka, maasi huongezeka; Bali wenye haki watayatazama maanguko yao. 17 Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako. 18 Pasipo maono, watu huacha kujizuia; Bali ana heri mtu yule aishikaye sheria. 19 Haitoshi mtumwa kuonywa kwa maneno; Maana ajapoyafahamu hataitika. 20 Je! Umemwona mtu mwenye kuhamaki katika maneno? Afadhali kumtumaini mpumbavu kuliko yeye. 21 Amtunduiaye mtumwa wake tangu utoto, Mwisho wake atakuwa ni mwanawe. 22 Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Na mtu mwenye ghadhabu huasi sana. 23 Kiburi cha mtu kitamshusha; Bali mwenye roho ya unyenyekevu ataheshimiwa. 24 Mshiriki wa mwivi huichukia nafsi yake mwenyewe; Asikia maapizo, wala hana neno. 25 Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; Bali amtumainiye Bwana atakuwa salama. 26 Watu wengi hutafuta upendeleo wa mkuu; Bali hukumu ya kila mtu hutoka kwa Bwana 27 Mtu aliye dhalimu ni chukizo kwa wenye haki; Na mnyofu wa mwenendo ni chukizo kwa waovu.

Mithali 30

1 Maneno ya Aguri bin Yake; mausia mtu huyu aliyomwambia Ithieli, naam, Ithieli na Ukali. 2 Hakika nimekuwa kama mnyama, wala si mtu; Wala sina ufahamu wa mwanadamu; 3 Wala sikujifunza hekima; Wala sina maarifa ya kumjua Mtakatifu. 4 Ni nani aliyepanda mbinguni na kushuka chini? Ni nani aliyekamata upepo kwa makonzi yake? Ni nani aliyeyafunga maji ndani ya nguo yake? Ni nani aliyefanya imara ncha zote za nchi? Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwanawe, kama wajua? 5 Kila neno la Mungu limehakikishwa; Yeye ni ngao yao wamwaminio. 6 Usiongeze neno katika maneno yake; Asije akakulaumu, ukaonekana u mwongo. 7 Mambo haya mawili nimekuomba; Usininyime matatu kabla sijafa. 8 Uniondolee ubatili na uongo; Usinipe umaskini wala utajiri; Unilishe chakula kilicho kadiri yangu. 9 Nisije nikashiba nikakukana, Nikasema, Bwana ni nani? Wala nisiwe maskini sana nikaiba, Na kulitaja bure jina la Mungu wangu. 10 Usimchongee mtumwa kwa bwana wake; Asije akakulaani, ukaonekana una hatia. 11 Kuna kizazi cha watu wamlaanio baba yao; Wala hawambariki mama yao. 12 Kuna kizazi cha watu walio safi machoni pao wenyewe; Ambao hawakuoshwa uchafu wao. 13 Kuna kizazi cha watu ambao macho yao yameinuka kama nini! Na kope zao zimeinuka sana. 14 Kuna kizazi cha watu ambao meno yao ni panga; Na vigego vyao ni kama visu. Ili kuwala maskini waondolewe katika nchi, Na wahitaji katika wanadamu. 15 Mruba anao binti wawili, Waliao, Nipe! Nipe! Kuna vitu vitatu visivyoshiba kamwe, Naam, vinne visivyosema, Basi! 16 Kuzimu; na tumbo lisilozaa; Nchi isiyoshiba maji; na moto usiosema, Basi! 17 Jicho la mtu amdhihakiye babaye, Na kudharau kumtii mamaye; Kunguru wa bondeni wataling'oa, Na vifaranga vya tai watalila. 18 Kuna mambo matatu yaliyo ya ajabu kwangu, Naam, kuna manne nisiyoyafahamu. 19 Mwendo wa tai katika hewa; Na mwendo wa nyoka juu ya mwamba; Mwendo wa merikebu katikati ya bahari; Na mwendo wa mtu pamoja na msichana. 20 Hivyo ndivyo mwendo wa mwanamke mzinifu; Hula, akapangusa kinywa chake, Akasema, Sikufanya uovu. 21 Kwa ajili ya mambo matatu nchi hutetemeka, Naam, kwa ajili ya manne haiwezi kuvumilia. 22 Mtumwa apatapo kuwa mfalme; Mpumbavu ashibapo chakula; 23 Mwanamke mwenye kuchukiza aolewapo; Na mjakazi aliye mrithi wa bibi yake. 24 Kuna viumbe vinne duniani vilivyo vidogo; Lakini vina akili nyingi sana. 25 Chungu ni watu wasio na nguvu; Lakini hujiwekea chakula wakati wa hari. 26 Wibari ni watu dhaifu; Lakini hujifanyia nyumba katika miamba. 27 Nzige hawana mfalme; Lakini huenda wote pamoja vikosi vikosi. 28 Mjusi hushika kwa mikono yake; Lakini yumo majumbani mwa wafalme. 29 Kuna watatu wenye mwendo wa kupendeza, Naam, wanne walio na mwendo mzuri. 30 Simba aliye hodari kupita wanyama wote; Wala hajiepushi na aliye yote; 31 Jimbi aendaye tambo; na beberu; Na mfalme ambaye haasiki. 32 Ikiwa umefanya kipumbavu kwa kujikuza; Au ikiwa umewaza mabaya; Basi weka mkono wako juu ya kinywa chako. 33 Kwa maana kupiga maziwa huleta siagi; Na kupiga pua hutokeza damu; kadhalika kuchochea hasira hutokeza ugomvi.

Mithali 31

1 Maneno ya mfalme Lemueli; mausia aliyofundishwa na mama yake. 2 Ni nini, mwanangu? Tena ni nini, mwana wa tumbo langu? Tena, ni nini mwana wa nadhiri zangu? 3 Usiwape wanawake nguvu zako; Wala moyo wako usiwape wale wawaharibuo wafalme. 4 Ee Lemueli, kunywa mvinyo hakuwafai wafalme, hakuwafai wafalme; Wala haifai wakuu waseme, Ki wapi kileo? 5 Wasije wakanywa na kuisahau sheria, Na kuipotosha hukumu ya mtu aliye taabuni. 6 Mpe kileo yeye aliye karibu na kupotea; Kampe divai yeye aliye na uchungu nafsini. 7 Anywe akausahau umaskini wake; Asiikumbuke tena taabu yake. 8 Fumbua kinywa chako kwa ajili yake aliye bubu; Uwatetee watu wote walioachwa peke yao; 9 Fumbua kinywa chako, uhukumu kwa haki; Uwapatie maskini na wahitaji haki yao. 10 Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana kima chake chapita kima cha marijani. 11 Moyo wa mumewe humwamini, Wala hatakosa kupata mapato. 12 Humtendea mema wala si mabaya, Siku zote za maisha yake. 13 Hutafuta sufu na kitani; Hufanya kazi yake ya mikono kwa moyo. 14 Afanana na merikebu za biashara; Huleta chakula chake kutoka mbali. 15 Tena huamka, kabla haujaisha usiku; Huwapa watu wa nyumbani mwake chakula; Na wajakazi wake sehemu zao. 16 Huangalia shamba, akalinunua; Kwa mapato ya mikono yake hupanda mizabibu. 17 Hujifunga nguvu viunoni kama mshipi; Hutia mikono yake nguvu. 18 Huona kama bidhaa yake ina faida; Taa yake haizimiki usiku. 19 Hutia mikono yake katika kusokota; Na mikono yake huishika pia. 20 Huwakunjulia maskini mikono yake; Naam, huwanyoshea wahitaji mikono yake. 21 Hawahofii theluji watu wa nyumbani mwake; Maana wote wa nyumbani mwake huvikwa nguo nyekundu. 22 Hujifanyia mazulia ya urembo; Mavazi yake ni kitani safi na urujuani. 23 Mume wake hujulikana malangoni; Aketipo pamoja na wazee wa nchi. 24 Hufanya nguo za kitani na kuziuza; Huwapa wafanya biashara mishipi. 25 Nguvu na hadhi ndiyo mavazi yake; Anaucheka wakati ujao. 26 Hufumbua kinywa chake kwa hekima, Na sheria ya wema i katika ulimi wake. 27 Huangalia sana njia za watu wa nyumbani mwake; Wala hali chakula cha uvivu. 28 Wanawe huondoka na kumwita heri; Mumewe naye humsifu, na kusema, 29 Binti za watu wengi wamefanya mema, Lakini wewe umewapita wote. 30 Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; Bali mwanamke amchaye Bwana, ndiye atakayesifiwa. 31 Mpe mapato ya mikono yake, Na matendo yake yamsifu malangoni.

Mhubiri 1

1 Maneno ya Mhubiri mwana wa Daudi,mfalme katika Yerusalemu. 2 Mhubiri asema, Ubatili mtupu, ubatili mtupu, mambo yote ni ubatili. 3 Mtu ana faida gani ya kazi yake yote aifanyayo chini ya jua? 4 Kizazi huenda, kizazi huja; nayo dunia hudumu daima. 5 Jua lachomoza, na jua lashuka, na kufanya haraka kwenda mahali pa maawio yake. 6 Upepo huvuma kusi, hugeuka kuwa kaskazi; hugeuka daima katika mwendo wake, na upepo huyarudia mazunguko yake. 7 Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena. 8 Mambo yote yamejaa uchovu usioneneka, jicho halishibi kuona, wala sikio halikinai kusikia. 9 Yaliyokuwako ndiyo yatakayokuwako; na yaliyotendeka ndiyo yatakayotendeka; wala jambo jipya hakuna chini ya jua. 10 Je! Kuna jambo lo lote ambalo watu husema juu yake, Tazama, ni jambo jipya? Limekwisha kuwako, tangu zamani za kale zilizokuwa kabla yetu sisi. 11 Hakuna kumbukumbu lo lote la vizazi vilivyotangulia; wala hakutakuwa na kumbukumbu lo lote la vizazi vitakavyokuja, miongoni mwao wale watakaofuata baadaye. 12 Mimi, Mhubiri, nalikuwa Mfalme wa Israeli katika Yerusalemu. 13 Nikatia moyo wangu ili kuyatafuta yote yanayotendeka chini ya mbingu, na kuyavumbua kwa hekima; ni taabu kubwa ambayo Mungu amewapa wanadamu, ili kutaabika ndani yake. 14 Nimeziona kazi zote zifanywazo chini ya jua; na, tazama, mambo yote ni ubatili na kujilisha upepo. 15 Yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa, Wala yasiyokuwapo hayahesabiki. 16 Nikatafakari nikisema, Nimejipatia hekima nyingi kupita wote walionitangulia katika Yerusalemu; naam, moyo wangu umeona kwa wingi hekima na maarifa. 17 Nikatia moyo wangu ili kuijua hekima, na kujua wazimu na upumbavu; nikatambua ya kwamba hayo yote nayo ni kujilisha upepo. 18 Yaani, Katika wingi wa hekima mna wingi wa huzuni,Naye aongezaye maarifa huongeza masikitiko.

Mhubiri 2

1 Nikauambia moyo wangu, Haya, nitakujaribu kwa njia ya furaha basi ujifurahishe kwa anasa. Na tazama, hayo nayo yakawa ubatili. 2 Nikasema juu ya kicheko, Ni wazimu; na juu ya furaha, Yafaa nini? 3 Moyoni mwangu nikapeleleza jinsi ya kuuburudisha mwili kwa mvinyo, na (moyo wangu ukali ukiniongoza kwa hekima) jinsi ya kushikana na upumbavu, hata niyaone yaliyo mema ya kuwafaa wanadamu, ili wayafanye hayo chini ya mbingu siku zote za maisha yao. 4 Nikajifanyizia kazi zilizo kubwa; nikajijengea nyumba; nikajipandia mashamba ya mizabibu; 5 nikajifanyizia bustani na viunga, na kuipanda humo miti yenye matunda ya kila namna; 6 nikajifanyizia birika za maji, ya kuunyweshea mwitu mlimopandwa miti michanga. 7 Nami nikanunua watumwa na wajakazi, nikawa na wazalia nyumbani mwangu; tena nikawa na mali nyingi za ng'ombe na kondoo, kupita wote walionitangulia katika Yerusalemu; 8 tena nikajikusanyia fedha na dhahabu, na tunu za kifalme na za kutoka katika majimbo. Nikajipatia waimbaji, waume kwa wake, nao wale ambao wanadamu wanawatunuka, masuria wengi sana. 9 Basi nikawa mkuu, nikaongezeka kupita wote walionitangulia katika Yerusalemu; pia hekima yangu nikakaa nayo. 10 Wala sikuyanyima macho yangu cho chote yalichokitamani; wala sikuuzuia moyo wangu katika furaha yo yote; maana moyo wangu ulifurahi kwa sababu ya kazi yangu yote, na hii ilikuwa sehemu yangu katika kazi yangu yote. 11 Kisha nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili na kujilisha upepo, wala faida hakuna chini ya jua. 12 Nikageuka ili kuipambanua hekima, na wazimu na upumbavu. Kwa maana mtu amfuataye mfalme afanye nini? Lilo hilo tu lililokwisha kufanywa. 13 Ndipo nilipoona ya kuwa kweli hekima hupita upumbavu, kwa kadiri nuru ipitavyo giza; 14 macho yake mwenye hekima yamo kichwani mwake, lakini mpumbavu huenda gizani; ila hata hivyo nikatambua ya kwamba ni tukio moja la mwisho liwapatalo wote sawasawa. 15 Nikasema moyoni mwangu, Kama limpatavyo mpumbavu, ndivyo litakavyonipata mimi nami; basi, kwa nini nikawa na hekima zaidi? Nikasema moyoni mwangu ya kuwa hayo nayo ni ubatili. 16 Maana hakuna kumbukumbu la milele la mwenye hekima, wala la mpumbavu; kwa sababu siku zijazo wote pia watakuwa wamekwisha kusahauliwa. Na mwenye hekima, jinsi gani anavyokufa sawasawa na mpumbavu! 17 Basi, nikauchukia uhai; kwa sababu kazi inayotendeka chini ya jua ilikuwa mbaya kwangu; yaani, mambo yote ni ubatili na kujilisha upepo. 18 Nami nikaichukia kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo chini ya jua; maana sina budi kumwachia yeye atakayenifuata. 19 Naye ni nani ajuaye kama huyo atakuwa mwenye hekima au mpumbavu? Hata hivyo atatawala juu ya kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo, ambamo ndani yake mimi nimeonyesha hekima chini ya jua. Hayo nayo ni ubatili. 20 Kwa hiyo nikageuka kukata tamaa moyoni mwangu juu ya kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo chini ya jua. 21 Maana kuna mtu ambaye kazi yake ni kwa hekima, na kwa maarifa, na kwa ustadi; naye atamwachia mtu asiyeshughulika nayo kuwa sehemu yake. Hayo tena ni ubatili, nayo ni baa kuu. 22 Kwa maana mtu hupata nini kwa kazi yake yote, na kwa juhudi ya moyo wake alivyojitahidi chini ya jua? 23 Kwa kuwa siku zake zote ni masikitiko, na kazi yake ni huzuni; naam, hata usiku moyoni mwake hamna raha. Hayo nayo ni ubatili. 24 Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha roho yake kwa mema katika kazi yake. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu. 25 Kwa maana ni nani awezaye kula au kujiburudisha kuliko mimi? 26 Kwa sababu Mungu humpa yeye aliyemridhia hekima na maarifa na furaha; bali mkosaji humpa taabu, ili kukusanya na kututa, apate kumpa huyo ambaye Mungu amridhia. Hayo nayo ni ubatili na kujilisha upepo.

Mhubiri 3

1 Kwa kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu. 2 Wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa; Wakati wa kupanda, na wakati wa kung'oa yaliyopandwa; 3 Wakati wa kuua, na wakati wa kupoza; Wakati wa kubomoa, na wakati wa kujenga; 4 Wakati wa kulia, na wakati wa kucheka; Wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza; 5 Wakati wa kutupa mawe, na wakati wa kukusanya mawe; Wakati wa kukumbatia, na wakati wa kutokumbatia; 6 Wakati wa kutafuta, na wakati wa kupoteza; Wakati wa kuweka, na wakati wa kutupa; 7 Wakati wa kurarua, na wakati wa kushona; Wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena; 8 Wakati wa kupenda, na wakati wa kuchukia; Wakati wa vita, na wakati wa amani. 9 Je! Mtendaji anayo faida gani katika yale anayojishughulisha nayo? 10 Nimeiona taabu ambayo Mungu amewapa wanadamu, ili kutaabika ndani yake. 11 Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho. 12 Mimi najua ya kwamba hakuna jema kwao kupita kufurahi, na kufanya mema maadamu wanaishi. 13 Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote. 14 Najua ya kwamba kila kazi aifanyayo Mungu itadumu milele; haiwezekani kuizidisha kitu, wala kuipunguza kitu; nayo Mungu ameifanya ili watu wamche Yeye. 15 Yale yaliyoko yamekuwako; na hayo yatakayokuwako yamekwisha kuwako; naye Mungu huyatafuta tena mambo yale yaliyopita. 16 Zaidi ya hayo, nikaona tena chini ya jua ya kwamba, Mahali pa hukumu upo uovu, Na mahali pa haki upo udhalimu. 17 Nikasema moyoni mwangu, Mungu atawahukumu wenye haki na wasio haki; kwa kuwa kuna wakati huko kwa kila kusudi na kwa kila kazi. 18 Nikasema moyoni mwangu, Ni kwa sababu ya wanadamu, ili Mungu awajaribu, nao waone ya kuwa wao wenyewe wafanana na wanyama. 19 Kwa maana linalowatukia wanadamu linawatukia wanyama; jambo moja lawatukia; anavyokufa huyu ndivyo anavyokufa huyu; naam, wote wanayo pumzi moja; wala mwanadamu hana kitu cha kumpita mnyama; kwa maana yote ni ubatili. 20 Wote huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena. 21 Ni nani ajuaye kama roho ya binadamu huenda juu, na kama roho ya mnyama huenda chini? 22 Hivyo nikaona ya kwamba hakuna jema kupita mwanadamu kuzifurahia kazi zake; kwa sababu hili ni fungu lake; kwa maana ni nani atakayemrudisha tena ili ayaone yatakayomfuata baadaye.

Mhubiri 4

1 Kisha nikarudi na kuona madhalimu yote yanayotendeka chini ya jua; na tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo, walakini wale walikuwa hawana mfariji. 2 Kwa hiyo nikawasifu wafu waliokwisha kufa kuliko wenye uhai walio hai bado; 3 naam, zaidi ya hao wote nikamwita heri yeye asiyekuwako bado, ambaye hakuyaona mabaya yanayotendeka chini ya jua. 4 Tena nikafikiri amali zote, na kila kazi ya ustadi, ya kwamba inatoka katika mtu kupingana na mwenzake. Hayo nayo ni ubatili na kujilisha upepo. 5 Mpumbavu huikunja mikono yake, Naye hula chakula chake mwenyewe; 6 Heri konzi moja pamoja na utulivu, Kuliko konzi mbili pamoja na taabu; na kujilisha upepo. 7 Kisha nikarudi tena, na kuona ubatili chini ya jua. 8 Kuna mtu aliye peke yake, wala hana wa pili wake; naam, hana mwana wala ndugu; hata hivyo amali yake haina mwisho, wala macho yake hayashibi utajiri. Basi asema, Ni kwa ajili ya nani nafanya kazi, na kujinyima nafsi yangu mema? Hayo nayo ni ubatili, naam, ni taabu kubwa. 9 Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja; Maana wapata ijara njema kwa kazi yao. 10 Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake; lakini ole wake aliye peke yake aangukapo, wala hana mwingine wa kumwinua! 11 Tena, wawili wakilala pamoja, hapo watapata moto; lakini mmoja aliye peke yake tu awezaje kuona moto? 12 Hata ikiwa mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake, wawili watampinga; wala kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi. 13 Heri kijana maskini mwenye hekima Kuliko mfalme mzee mpumbavu. 14 Kwa maana kutoka gerezani alikuja kumiliki; naam, hata katika ufalme wake alizaliwa hali ya umaskini. 15 Nikawaona wote walio hai waendao chini ya jua, ya kwamba walishikamana na huyo kijana, huyo wa pili aliyesimama badala ya yule. 16 Hawakuwa na kikomo hao watu wote, hao wote ambao alikuwa juu yao; lakini hata hivyo wale wafuatao baada yake hawatamfurahia. Hakika hayo pia ni ubatili, na kujilisha upepo.

Mhubiri 5

1 Jitunze mguu wako uendapo nyumbani kwa Mungu; Maana ni heri kukaribia ili usikie, Kuliko kutoa kafara ya wapumbavu; Ambao hawajui kuwa wafanya mabaya. 2 Usiseme maneno ya ujinga kwa kinywa chako, wala moyo wako usiwe na haraka kunena mbele za Mungu; kwa maana, Mungu yuko mbinguni, na wewe upo chini, Kwa hiyo maneno yako na yawe machache. 3 Kwa maana ndoto huja kwa sababu ya shughuli nyingi; na sauti ya mpumbavu kwa njia ya wingi wa maneno. 4 Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri. 5 Ni afadhali usiweke nadhiri, Kuliko kuiweka usiiondoe. 6 Usikiache kinywa chako kuukosesha mwili wako; wala usiseme mbele ya huyo malaika ya kwamba umepitiliwa; kwani Mungu akukasirikie sauti yako, na kuiharibu kazi ya mikono yako? 7 Maana ndivyo ilivyo katika habari za wingi wa ndoto, na ubatili, na maneno mengi; walakini wewe umche Mungu. 8 Ujapokuwa unaona maskini kuonewa, na hukumu na haki kuondolewa kwa jeuri katika jimbo, usilistaajabie jambo hilo; kwa sababu, Aliye juu kuliko walio juu huangalia; Tena wako walio juu kupita hao. 9 Lakini, pamoja na hayo, manufaa ya nchi kwa kila njia ni mfalme anayejibidiisha kwa ajili ya shamba. 10 Apendaye fedha hatashiba fedha, Wala apendaye wingi hatashiba maongeo. Hayo pia ni ubatili. 11 Mali yakiongezeka, hao walao nao waongezeka na mwenyewe hufaidiwa nini, ila kuyatazama kwa macho yake tu? 12 Usingizi wake kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi; lakini kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi. 13 Kuna na balaa mbaya sana niliyoiona chini ya jua, nayo ni hii, mali alizoziweka mwenyewe kwa kujinyima; 14 na mali hizo zimepotea kwa bahati mbaya; naye akiwa amezaa mwana, hamna kitu mkononi mwake. 15 Alivyotoka tumboni mwa mamaye, atakwenda tena tupu-tupu kama alivyokuja; asichume kitu cho chote kwa ajili ya kazi yake, hata akichukue mkononi mwake. 16 Hiyo ndiyo balaa mbaya sana, ya kwamba kama vile alivyokuja, vivyo hivyo atakwenda zake; naye amefaidiwa nini mwenye kujitaabisha kwa ajili ya upepo? 17 Siku zake zote hula gizani, mwenye fadhaa nyingi, mwenye ugonjwa na uchungu. 18 Tazama, mimi niliyoyaona kuwa ndiyo mema na ya kufaa, ni mtu kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote anayoifanya chini ya jua, siku zote za maisha yake alizopewa na Mungu; maana hilo ndilo fungu lake. 19 Tena, kwa habari za kila mwanadamu, ambaye Mungu amempa mali na ukwasi, akamwezesha kula katika hizo, na kuipokea sehemu yake, na kuifurahia amali yake; hiyo ndiyo karama ya Mungu. 20 Kwa kuwa mtu hatazikumbuka mno siku za maisha yake; kwa sababu Mungu humtakabali katika furaha ya moyo wake.

Mhubiri 6

1 Kuna baa nililoliona mimi chini ya jua, nalo linawalemea wanadamu kwa uzito; 2 mtu aliyepewa na Mungu mali, ukwasi, na heshima, hata asipungukiwe na kitu cho chote kwa nafsi yake, katika yote anayoyatamani walakini Mungu hamwezeshi kula katika hizo; bali mgeni hula. Hayo ndiyo ubatili hasa, nayo ni ugonjwa mbaya. 3 Mtu akizaa watoto mia, akaishi miaka mingi, nazo siku za maisha yake ni nyingi, lakini nafsi yake haikushiba mema; tena ikiwa, zaidi ya hayo, amekosa maziko; mimi nasema, Heri mimba iliyoharibika kuliko huyo; 4 yaani, hiyo huja katika ubatili, na huenda gizani, nalo jina lake limefunikwa giza; 5 tena, haikuliona jua wala kulifahamu; basi, hii imepata kustarehe kuliko yule; 6 naam, ajapoishi miaka elfu mara mbili, asijiburudishe kwa mema; je! Wote hawaendi mahali pamoja? 7 Kazi yote ya binadamu ni kwa kinywa chake, Walakini hata hivyo nafsi yake hashibi. 8 Kwa maana mwenye hekima hupata faida gani kuliko mpumbavu? Au maskini ana nini kuliko yeye ajuaye kwenda mbele ya walio hai? 9 Heri kuona kwa macho, Kuliko kutanga-tanga kwa tamaa. Hayo nayo ni ubatili, na kujilisha upepo. 10 Na awe kitu cho chote, aliitwa jina lake zamani za kale, naye amejulikana kuwa ndiye mwanadamu; wala hawezi kabisa kushindana na yeye aliye na uwezo kuliko yeye mwenyewe. 11 Basi, kwa kuwa kuna mambo mengi yaongezayo ubatili, mwanadamu hufaidiwa nini? 12 Kwa maana ni nani ajuaye yaliyo mema ya mwanadamu katika maisha yake, siku zote za maisha yake ya ubatili, anayoishi kama kivuli? Kwa maana ni nani awezaye kumweleza mwanadamu mambo yatakayofuata baada yake chini ya jua?

Mhubiri 7

1 Heri sifa njema kuliko marhamu nzuri; Na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa. 2 Heri kuiendea nyumba ya matanga, Kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kwa maana huo ndio mwisho wa wanadamu wote, naye aliye hai atautia moyoni mwake. 3 Huzuni ni afadhali kuliko kicheko, Maana simanzi ya uso ni faida ya moyo. 4 Moyo wake mwenye hekima umo nyumbani mwa matanga, bali moyo wake mpumbavu umo nyumbani mwa furaha. 5 Heri kusikia laumu ya wenye hekima, Kuliko mtu kusikia wimbo wa wapumbavu; 6 Maana kama mlio wa miiba chini ya sufuria, Ndivyo kilivyo kicheko cha mpumbavu. Hayo nayo ni ubatili. 7 Kweli jeuri humpumbaza mwenye hekima, Na rushwa huuharibu ufahamu. 8 Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake, Na mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi. 9 Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, Maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu. 10 Usiseme, Kwani siku za kale kupita siku hizi? Maana si kwa hekima uulizavyo neno hilo. 11 Hekima ni njema, mfano wa urithi; Naam, nayo ni bora kwao walionao jua. 12 Kwa maana hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo. 13 Tafakari vema kazi yake Mungu; kwa sababu ni nani awezaye kukinyosha kitu kile alichokipotosha yeye? 14 Siku ya kufanikiwa ufurahi, Na siku ya mabaya ufikiri. Mungu ameifanya hiyo moja kwenda sambamba na hiyo ya pili, ili mwanadamu asipate kulijua neno lo lote litakalofuata baada yake. 15 Mambo hayo yote nimeyaona mimi katika siku za ubatili wangu, yuko mwenye haki apoteaye katika haki yake, yuko na mtu mwovu azidishaye maisha yake katika udhalimu wake. 16 Usiwe na haki kupita kiasi; Wala usijiongezee hekima mno; Kwani kujiangamiza mwenyewe? 17 Usiwe mwovu kupita kiasi; Wala usiwe mpumbavu; Kwani ufe kabla ya wakati wako? 18 Ni vizuri kwamba ulishike neno hilo; naam, hata kwa neno hilo tena usiuondoe mkono wako; kwa kuwa mtu yule amchaye Mungu atatoka katika hayo yote. 19 Hekima ni nguvu zake mwenye hekima, Zaidi ya wakuu kumi waliomo mjini. 20 Bila shaka hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani, ambaye afanya mema, asifanye dhambi. 21 Tena, usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa; usije ukamsikia mtumwa wako mwenyewe ali anakutukana. 22 Kwa kuwa mara nyingi moyo wako pia unajua ya kwamba wewe mwenyewe umewatukana watu wengine. 23 Mambo hayo yote mimi nimeyahakikisha katika hekima. Nilisema, Mimi nitakuwa na hekima, lakini imefarakana nami. 24 Mambo yale yaliyo mbali, na yale yaendayo chini sana, ni mtu yupi awezaye kuyatafuta? 25 Nikageuka, na moyo wangu ulikazwa katika kujua na kupeleleza, na kuitafuta hekima, na maana ya mambo yaliyoko; ili nifahamu ya kuwa uovu ni upumbavu, na upumbavu ni wazimu. 26 Nami nimeona lililo na uchungu kupita mauti; yaani, mwanamke ambaye moyo wake ni mitego na tanzi, na mikono yake ni kama vifungo; yeye ampendezaye Mungu atamponyoka, bali mwenye dhambi atanaswa na yeye. 27 Tazama, asema Mhubiri, mimi nimeyaona hayo kwa kulinganisha hili na hili, ili kuitafuta jumla; 28 ambayo bado nafsi yangu nikali nikiitafuta, nisiione; mwanamume mmoja katika elfu nimemwona; bali mwanamke mmoja miongoni mwa wote mimi sikumwona. 29 Tazama, hili tu nimeliona; Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu, lakini wamebuni mavumbuzi mengi.

Mhubiri 8

1 Ni nani aliye kama mwenye hekima; Naye ni nani ajuaye kufasiri neno? Hekima ya mtu humng'ariza uso wake, Na ugumu wa uso wake hubadilika. 2 Mimi nasema hivi, Uishike amri ya mfalme; na hiyo kwa sababu umeapa kwa Mungu. 3 Usifanye haraka kutoka mbele ya uso wake; usiendelee kufanya lililo baya; maana yeye hufanya lo lote limpendezalo. 4 Kwa kuwa neno la mfalme lina nguvu; naye ni nani awezaye kumwambia huyo, Wafanya nini? 5 Aishikaye amri hatajua neno baya; Na moyo wa mwenye hekima hujua wakati na hukumu. 6 Kwa maana kwa kila shauri kuna wakati na hukumu; kwa sababu mashaka ya mwanadamu yaliyo juu yake ni makubwa; 7 kwa kuwa hajui yatakayokuwako; kwa maana ni nani awezaye kumweleza jinsi yatakavyokuwa? 8 Hakuna mwenye uwezo juu ya roho aizuie roho; Wala hana mamlaka juu ya siku ya kufa; Wala hakuna kuruhusiwa katika vita vile; Wala uovu hautamwokoa yule aliyeuzoea. 9 Mambo hayo yote nimeyaona, nikatia moyo wangu katika kila kazi iliyofanyika chini ya jua. Kuna wakati ambapo mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasira yake. 10 Pia nikaona waovu wamezikwa, nao wamefika kaburini; tena waliofanya mema wameondoka katika patakatifu, nao wamesahauliwa mjini. Hayo nayo ni ubatili. 11 Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya. 12 Ajapokuwa mwenye dhambi amefanya maovu mara mia, akazidisha siku zake; lakini hata hivyo najua hakika ya kwamba itakuwa heri kwao wamchao Mungu, wenye kicho mbele zake; 13 walakini haitakuwa heri kwa mwovu, wala hatazidisha siku zake, zilizo kama kivuli; kwa sababu hana kicho mbele za Mungu. 14 Kuna ubatili unaofanyika juu ya nchi, kwamba wako wenye haki nao wapatilizwa kama kwa kazi yao waovu; tena wako waovu, nao wapatilizwa kama kwa kazi yao wenye haki. Nami nikasema ya kuwa hayo nayo ni ubatili. 15 Kisha nikaisifu furaha, kwa sababu mwanadamu hana neno lo lote lililo jema chini ya jua, kuliko kula, na kunywa, na kucheka; na yakuwa hilo likae naye katika amali yake, siku zote za maisha yake alizompa Mungu chini ya jua. 16 Mimi nilipotia moyo wangu katika kuijua hekima, na kuuona utumishi uliofanyika juu ya nchi, (maana kuna asiyepata usingizi kwa macho yake mchana wala usiku); 17 basi, niliiona kazi yote ya Mungu, ya kuwa haitafutikani na mwanadamu kazi inayofanyika chini ya jua; kwa sababu mwanadamu na akijisumbua kadiri awezavyo kuitafuta, hata hivyo hataiona; naam, zaidi ya hayo, mwenye hekima ajapodhania ya kuwa ataijua, lakini yeye hataweza kuiona.

Mhubiri 9

1 Na kwa ajili ya hayo yote, nikatia moyo wangu katika kuyatafuta-tafuta haya; ya kuwa wenye haki, na wenye hekima, pamoja na matendo yao yote, wamo mkononi mwa Mungu; kwamba ni pendo au kwamba ni chuki, mwanadamu hajui; mambo yote yawapita. 2 Mambo yote yawatukia wote sawasawa; kuna tukio moja kwake mwenye haki na kwake asiye haki; kwa mtu mwema na kwa mtu mwovu; kwa mtu aliye safi na kwa mtu asiye safi; kwake yeye atoaye kafara na kwake asiyetoa kafara; kama alivyo huyo mwema ndivyo alivyo mwenye dhambi; yeye aapaye na yeye aogopaye kiapo. 3 Baa hilo ni katika mambo yote yanayofanyika chini ya jua, ya kuwa wote wanalo tukio moja; naam, zaidi ya hayo, mioyo ya wanadamu imejaa maovu, na wazimu umo mioyoni mwao wakati walipo hai, na baadaye huenda kwa wafu. 4 Kwa kuwa liko tumaini kwa yule aliyeambatana na wote walio hai; (maana ni afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa); 5 kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa. 6 Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja; wala hawana sehemu tena katika jambo lo lote lililofanyika chini ya jua. 7 Wewe enenda zako, ule chakula chako kwa furaha, unywe mvinyo yako kwa moyo wa kuchangamka; kwa kuwa Mungu amekwisha kuzikubali kazi zako. 8 Mavazi yako na yawe meupe sikuzote; wala kichwa chako kisikose marhamu. 9 Uishi kwa furaha pamoja na mke umpendaye, siku zote za maisha yako ya ubatili, ulizopewa chini ya jua; siku zote za ubatili wako, kwa maana huo ni sehemu yako ya maisha; na katika taabu zako ulizozitaabika chini ya jua. 10 Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe. 11 Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati huwapata wote. 12 Maana mwanadamu naye hajui wakati wake; kama samaki wanaokamatwa katika nyavu mbaya, na mfano wa ndege wanaonaswa mtegoni, kadhalika wanadamu hunaswa katika wakati mbaya, unapowaangukia kwa ghafula. 13 Pia nimeona hekima chini ya jua, nayo ni kama hivi, tena kwangu mimi ilionekana kuwa ni neno kubwa. 14 Palikuwa na mji mdogo, na watu ndani yake walikuwa wachache; akaja mfalme mkuu juu yake, akauhusuru, akajenga ngome kubwa ili kuupiga. 15 Basi, kulionekana humo mtu maskini mwenye hekima, naye kwa hekima yake akauokoa mji ule lakini hata hivyo hapakuwa na mtu ye yote aliyemkumbuka yule mtu maskini. 16 Ndipo niliposema, Bora hekima kuliko nguvu; walakini hekima ya maskini hudharauliwa, wala maneno yake hayasikilizwi. 17 Maneno ya wenye hekima yanenwayo taratibu husikiwa, Zaidi ya mlio wake atawalaye katikati ya wapumbavu. 18 Hekima ndiyo bora kupita silaha za vita; Lakini mkosaji mmoja huharibu mema mengi.

Mhubiri 10

1 Mainzi mafu huvundisha marhamu ya mwuza marashi; Kadhalika upumbavu haba ni mzito kuliko hekima na heshima. 2 Moyo wake mwenye hekima upo upande wa kuume; Bali moyo wake mpumbavu upo mkono wa kushoto. 3 Naam, huyo mpumbavu tena, aendapo njiani, hupungukiwa na fahamu zake; hata humwambia kila mtu ya kuwa yeye ni mpumbavu. 4 Roho yake mtawala ikiinuka kinyume chako, Usiondoke mara mahali pako ulipo; Kwa maana roho ya upole hutuliza machukizo yaliyo makubwa. 5 Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye; 6 ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi hukaa mahali pa chini. 7 Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa. 8 Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake; Na yeye abomoaye boma, nyoka atamwuma. 9 Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo; Naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo. 10 Iwapo chuma hakipati, wala mtu hakinoi; Ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi. Walakini yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa. 11 Nyoka akiuma asijatumbuizwa, Basi hakuna faida ya mtumbuizi. 12 Maneno ya kinywa chake mwenye hekima yana neema; Bali midomo ya mpumbavu itammeza nafsi yake. 13 Mwanzo wa maneno ya kinywa chake ni upuuzi; na mwisho wa usemi wake ni wazimu wenye hatari. 14 Tena, upumbavu huongeza maneno; lakini mwanadamu hajui yatakayokuwako; nayo yatakayokuwa baada yake, ni nani awezaye kumweleza? 15 Kazi yao wapumbavu huwachosha kila mmoja, Maana hajui hata njia ya kuuendea mji. 16 Ole wako, nchi, akiwa mfalme wako ni kijana, Na wakuu wako hula asubuhi! 17 Heri kwako, nchi, mfalme wako akiwa mtoto wa watu, Na wakuu wako hula wakati ufaao, Ili makusudi wapate nguvu, wala si kwa ajili ya ulevi. 18 Kwa sababu ya uvivu paa hunepa; Na kwa utepetevu wa mikono nyumba huvuja. 19 Karamu hufanywa kwa ajili ya kicheko, Na divai huyafurahisha maisha; Na fedha huleta jawabu la mambo yote. 20 Usimlaani mfalme, la, hata katika wazo lako; Wala usiwalaani wakwasi chumbani mwako; Kwa kuwa ndege wa anga ataichukua sauti, Na mwenye mabawa ataitoa habari.

Mhubiri 11

1 Tupa chakula chako usoni pa maji; Maana utakiona baada ya siku nyingi. 2 Uwagawie sehemu watu saba, hata wanane; Maana hujui baa gani litakalokuwa juu ya nchi. 3 Mawingu yakiwa yamejaa mvua, Yataimimina juu ya nchi; Na mti ukianguka kuelekea kusini, au kaskazini, Paangukapo ule mti, papo hapo utalala. 4 Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna. 5 Kama vile wewe usipojua njia ya upepo ni ipi, wala jinsi mifupa ikuavyo tumboni mwake mja mzito; kadhalika huijui kazi ya Mungu, afanyaye mambo yote. 6 Asubuhi panda mbegu zako, Wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa,kama ni hii au hii,au kama zote zitafaa sawasawa. 7 Kweli nuru ni tamu, tena ni jambo la kupendeza macho kutazama jua. 8 Naam, mtu akiishi miaka mingi, na aifurahie yote; lakini na azikumbuke siku zijazo za giza, kwa maana zitakuwa nyingi. Mambo yote yajayo ni ubatili. 9 Wewe kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako, lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni. 10 Kwa hiyo ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako; kwa maana ujana ni ubatili, na utu uzima pia.

Mhubiri 12

1 Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, Kabla hazijaja siku zilizo mbaya, Wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo. 2 Kabla jua, na nuru, na mwezi, Na nyota, havijatiwa giza; Kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua; 3 Siku ile walinzi wa nyumba watakapotetema; Hapo wenye nguvu watakapojiinamisha; Na wasagao kukoma kwa kuwa ni haba; Na hao wachunguliao madirishani kutiwa giza; 4 Na milango kufungwa katika njia kuu; Sauti ya kinu itakapokuwa ni ndogo; Na mtu kusituka kwa sauti ya ndege; Nao binti za kuimba watapunguzwa; 5 Naam, wataogopa kilichoinuka Na vitisho vitakuwapo njiani; Na mlozi utachanua maua; Na panzi atakuwa ni mzigo mzito; Na pilipili hoho itapasuka; Maana mtu aiendea nyumba yake ya milele, Nao waombolezao wazunguka njiani. 6 Kabla haijakatika kamba ya fedha; Au kuvunjwa bakuli la dhahabu; Au mtungi kuvunjika kisimani; Au gurudumu kuvunjika birikani; 7 Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, Nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa. 8 Mhubiri asema, Ubatili mtupu; mambo yote ni ubatili! 9 Walakini, kwa sababu huyo Mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa, naam, akatafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi. 10 Huyo Mhubiri akatafuta-tafuta ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli. 11 Maneno yao wenye hekima huwa mfano wa michokoo; na kama misumari iliyogongomewa sana; ndivyo yalivyo maneno yao walio wakuu wa makusanyiko, ambayo yatoka kwa mchungaji mmoja. 12 Tena, zaidi ya hayo, mwanangu, kubali maonyo; hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili. 13 Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, Maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. 14 Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.

Wimbo Ulio Bora 1

1 Wimbo ulio bora, wa Sulemani. 2 Kubusu na anibusu kwa kinywa chake. Maana pambaja zako zapita divai; 3 Manukato yako yanukia vizuri; Jina lako ni kama marhamu iliyomiminwa; Kwa hiyo wanawali hukupenda. 4 Nivute nyuma yako, na tukimbie; Mfalme ameniingiza vyumbani mwake. Tutafurahi na kukushangilia; Tutazinena pambaja zako kuliko divai; Ndiyo, ina haki wakupende. 5 Mimi ni mweusi-mweusi, lakini ninao uzuri, Enyi binti za Yerusalemu, Mfano wa hema za Kedari, Kama mapazia yake Sulemani. 6 Msinichunguze kwa kuwa ni mweusi-mweusi, Kwa sababu jua limeniunguza. Wana wa mamangu walinikasirikia, Waliniweka niwe mlinzi wa mashamba ya mizabibu; Bali shamba langu mwenyewe sikulilinda. 7 Nijulishe, ee mpendwa wa nafsi yangu, Ni wapi utakapolisha kundi lako, Ni wapi utakapolilaza adhuhuri. Kwa nini niwe kama aliyefungiwa kidoto, Karibu na makundi ya wenzako? 8 Usipojua, wewe uliye mzuri katika wanawake, Shika njia uzifuate nyayo za kondoo, Na kuwalisha wana-mbuzi wako Karibu na hema za wachungaji. 9 Mpenzi wangu, nimekulinganisha Na farasi katika magari ya Farao. 10 Mashavu yako ni mazuri kwa mashada, Shingo yako kwa mikufu ya vito. 11 Tutakufanyizia mashada ya dhahabu, Yenye vifungo vya fedha. 12 Muda mfalme alipoketi juu ya matakia, Nardo yangu ilitoa harufu yake. 13 Mpendwa wangu ni kama mfuko wa manemane Ukilazwa usiku maziwani mwangu. 14 Mpendwa wangu ni kama kishada cha hina, Katika mizabibu huko Engedi. 15 Tazama, u mzuri, mpenzi wangu, U mzuri, macho yako ni kama ya hua. 16 Tazama, u mzuri, mpendwa wangu, Wapendeza, na kitanda chetu ni majani; 17 Nguzo za nyumba yetu ni mierezi, Na viguzo vyetu ni miberoshi.

Wimbo Ulio Bora 2

1 Mimi ni ua la uwandani, Ni nyinyoro ya mabondeni. 2 Kama nyinyoro kati ya miiba, Kadhalika mpenzi wangu kati ya binti. 3 Kama mpera kati ya miti ya msituni, Kadhalika mpendwa wangu kati ya vijana. Naliketi kivulini mwake kwa furaha, Na matunda yake naliyaonja kuwa matamu. 4 Akanileta mpaka nyumba ya karamu, Na bendera yake juu yangu ni mapenzi. 5 Nishibisheni zabibu, niburudisheni kwa mapera, Kwa maana nimezimia kwa mapenzi. 6 Mkono wake wa kushoto uko chini ya kichwa changu, Nao wa kuume unanikumbatia! 7 Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, Kwa paa na kwa ayala wa porini, Msiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, Hata yatakapoona vema yenyewe. 8 Sikiliza! Ni mpendwa wangu! Tazama, anakuja, Akiruka milimani, akichachawa vilimani. 9 Mpendwa wangu ni kama paa, au ayala. Tazama, asimama nyuma ya ukuta wetu, Achungulia dirishani, atazama kimiani. 10 Mpendwa wangu alinena, akaniambia, Ondoka, mpenzi wangu, mzuri wangu, uje zako, 11 Maana tazama, kaskazi imepita, Masika imekwisha, imekwenda zake; 12 Maua yatokea katika nchi, Wakati wa kupelea umefika, Na sauti ya mwigo husikiwa kwetu. 13 Mtini wapevusha tini zake, Na mizabibu inachanua, Inatoa harufu yake nzuri; Ondoka, mpenzi wangu, mzuri wangu, uje zako. 14 Hua wangu, mafichoni mwa jabali, Katika sitara za magenge, Nitazame uso wako, nisikie sauti yako, Maana sauti yako ni tamu na uso wako mzuri. 15 Tukamatie mbweha, Wale mbweha wadogo, Waiharibuo mizabibu, Maana mizabibu yetu yachanua. 16 Mpendwa wangu ni wangu, na mimi ni wake; Hulisha kundi lake penye nyinyoro. 17 Hata jua lipunge, na vivuli vikimbie, Unigeukie, mpendwa wangu, Nawe uwe kama paa, au ayala, Juu ya milima ya Betheri.

Wimbo Ulio Bora 3

1 Usiku kitandani nalimtafuta mpendwa wa nafsi yangu, Nalimtafuta, nisimpate. 2 Nikasema, Haya, niondoke nizunguke mjini, Katika njia zake na viwanjani, Nimtafute mpendwa wa nafsi yangu. Nikamtafuta, nisimpate. 3 Walinzi wazungukao mjini waliniona; Je! Mmemwona mpendwa wa nafsi yangu? 4 Kitambo kidogo tu nikiisha kuwaondokea, Nikamwona mpendwa wa nafsi yangu; Nikamshika, nisimwache tena, Hata nilipomleta nyumbani mwa mamangu, Chumbani mwake aliyenizaa. 5 Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, Kwa paa na kwa ayala wa porini, Msiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, Hata yatakapoona vema yenyewe. 6 Ni nani huyu apandaye kutoka nyikani, Mfano wake ni nguzo za moshi; Afukizwa manemane na ubani, Na mavumbi ya manukato yote ya mchuuzi? 7 Tazama, ni machela yake Sulemani; Mashujaa sitini waizunguka, Wa mashujaa wa Israeli. 8 Wote wameshika upanga, Wamehitimu kupigana; Kila mtu anao upanga wake pajani Kwa hofu ya kamsa za usiku. 9 Mfalme Sulemani alijifanyizia machela Ya miti ya Lebanoni; 10 Nguzo zake alizifanyiza za fedha, Na mgongo wake wa dhahabu, Kiti chake kimepambwa urujuani, Gari lake limenakishiwa njumu, Hiba ya binti za Yerusalemu. 11 Tokeni, enyi binti za Sayuni, Mtazameni Mfalme Sulemani, Amevaa taji alivyovikwa na mamaye, Siku ya maposo yake, Siku ya furaha ya moyo wake.

Wimbo Ulio Bora 4

1 Tazama, u mzuri, mpenzi wangu, U mzuri, macho yako ni kama ya hua, Nyuma ya barakoa yako. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi, Wakijilaza mbavuni pa mlima Gileadi. 2 Meno yako ni kama kundi waliokatwa manyoya, Wakipanda kutoka kuoshwa, Ambao kila mmoja amezaa mapacha, Wala hakuna aliyefiwa kati yao. 3 Midomo yako ni kama uzi mwekundu, Na kinywa chako ni kizuri; Mashavu yako ni kama kipande cha komamanga, Nyuma ya barakoa yako. 4 Shingo yako ni kama mnara wa Daudi, Uliojengwa pa kuwekea silaha; Ngao elfu zimetungikwa juu yake, Zote ni ngao za mashujaa. 5 Maziwa yako mawili ni kama wana-paa wawili, Nyuma ya barakoa yako. Ambao ni mapacha ya paa; Wakilisha penye nyinyoro. 6 Hata jua lipunge, na vivuli vikimbie, Nitakwenda kwenye mlima wa manemane, Na kwenye kilima cha ubani. 7 Mpenzi wangu, u mzuri pia pia, Wala ndani yako hamna ila. 8 Bibi arusi, njoo pamoja nami toka Lebanoni, Pamoja nami toka Lebanoni. Shuka kutoka kilele cha Amana, Kutoka vilele vya Seniri na Hermoni; Kutoka mapangoni mwa simba, Kutoka milimani mwa chui. 9 Umenishangaza moyo, umbu langu, Bibi arusi, umenishangaza moyo, Kwa mtupo mmoja wa macho yako, Kwa mkufu mmoja wa shingo yako. 10 Jinsi zilivyo nzuri pambaja zako, umbu langu, Bibi arusi, ni nzuri kupita divai; Na harufu ya marhamu yako Yapita manukato ya kila namna. 11 Bibi arusi, midomo yako yadondoza asali, Asali na maziwa vi chini ya ulimi wako; Na harufu ya mavazi yako Ni kama harufu ya Lebanoni. 12 Bustani iliyofungwa ni umbu langu, bibi arusi, Kijito kilichofungwa, chemchemi iliyotiwa muhuri. 13 Machipuko yako ni bustani ya komamanga, Yenye matunda mazuri, hina na nardo, 14 Nardo na zafarani, mchai na mdalasini, Na miti yote iletayo ubani, Manemane na udi, na kolezi kuu zote. 15 Wewe ndiwe chemchemi ya bustani yangu, Kisima cha maji yaliyo hai, Vijito vya Lebanoni viendavyo kasi. 16 Amka, kaskazi; nawe uje, kusi; Vumeni juu ya bustani yangu, Manukato ya bustani yatokee. Mpendwa wangu na aingie bustanini mwake, Akayale matunda yake mazuri.

Wimbo Ulio Bora 5

1 Naingia bustanini mwangu, umbu langu, bibi arusi, Nachuma manemane yangu na rihani, Nala sega la asali na asali yangu, Nanywa divai yangu na maziwa. Kaleni, rafiki zangu, kanyweni, Naam, nyweni sana, wapendwa wangu. 2 Nalikuwa nimelala, lakini moyo wangu u macho, Sikiliza! Mpendwa wangu anabisha! Nifungulie, umbu langu, mpenzi wangu, Hua wangu, mkamilifu wangu, Kwa maana kichwa changu kimelowa umande, Nywele zangu zina manyunyu ya usiku. 3 Nimeivua kanzu yangu; niivaeje? Nimeitawadha miguu; niichafueje? 4 Mpendwa wangu aliutia mkono wake tunduni, Na moyo wangu ukachomeka kwa ajili yake. 5 Nikaondoka nimfungulie mpendwa wangu; Mikono yangu ilidondoza manemane, Na vidole vyangu matone ya manemane, Penye vipini vya komeo. 6 Nalimfungulia mpendwa wangu, Lakini mpendwa wangu amegeuka amepita; (Nimezimia nafsi yangu aliponena), Nikamtafuta, nisimpate, Nikamwita, asiniitikie. 7 Walinzi wazungukao mjini waliniona, Wakanipiga na kunitia jeraha, Walinzi walindao kuta zake Wakaninyang'anya shela yangu. 8 Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, Ninyi mkimwona mpendwa wangu, Ni nini mtakayomwambia? Ya kwamba nazimia kwa mapenzi. 9 Mpendwa wa namna gani ni mpendwa wako, Wewe uliye mzuri katika wanawake, Mpendwa wa namna gani ni mpendwa wako, Hata wewe utusihi hivyo? 10 Mpendwa wangu ni mweupe, tena mwekundu, Mashuhuri miongoni mwa elfu kumi; 11 Kichwa chake ni kama dhahabu safi sana, Nywele zake ni za ukoka, nyeusi kama kunguru; 12 Macho yake ni kama hua penye vijito, Wakioga kwa maziwa, wakiikalia mito iliyojaa; 13 Mashavu yake ni kama matuta ya rihani, Ambayo hufanyizwa manukato; Midomo yake ni kama nyinyoro, Inadondoza matone ya manemane; 14 Mikono yake ni kama mianzi ya dhahabu, lliyopambwa kwa zabarajadi; Kiwiliwili chake kama kazi ya pembe, Iliyonakishiwa kwa yakuti samawi; 15 Miguu yake ni kama nguzo za marimari, Zilizowekwa juu ya misingi ya dhahabu; Sura yake ni kama Lebanoni, Ni bora mfano wa mierezi; 16 Kinywa chake kimejaa maneno matamu, Ndiye mzuri sana pia pia. Ni huyu mpendwa wangu, ni huyu rafiki yangu, Enyi binti za Yerusalemu.

Wimbo Ulio Bora 6

1 Mpendwa wako amekwenda wapi, Wewe uliye mzuri katika wanawake? Mpendwa wako amegeukia upande upi, Ili tumtafute pamoja nawe? 2 Mpendwa wangu ameshukia bustani yake, Kwenye matuta ya rihani; Ili kulisha penye bustani, Ili kuchuma nyinyoro. 3 Mimi ni wake mpendwa wangu, naye ni wangu, Hulisha kundi lake penye nyinyoro. 4 Mpenzi wangu, u mzuri kama Tirza, Mwenye kupendeza kama Yerusalemu, Wa kutisha kama wenye bendera. 5 Uyageuzie macho yako mbali nami, Kwa maana yamenitisha sana. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi, Wakijilaza mbavuni pa Gileadi. 6 Meno yako kama kundi la kondoo, Wakipanda kutoka kuoshwa; Ambao kila mmoja amezaa mapacha, Wala hakuna aliyefiwa kati yao. 7 Mashavu yako ni kama kipande cha komamanga, Nyuma ya barakoa yako. 8 Wako malkia sitini, na masuria themanini, Na wanawali wasiohesabika; 9 Hua wangu, mkamilifu wangu, ni mmoja tu, Mtoto wa pekee wa mamaye. Ndiye kipenzi chake aliyemzaa, Binti wakamwona wakamwita heri; Malkia na masuria nao wakamwona, Wakamsifu, wakisema, 10 Ni nani huyu atazamaye kama alfajiri, Mzuri kama mwezi, safi kama jua, Wa kutisha kama wenye bendera? 11 Nalishukia bustani ya milozi, Ili kuyatazama machipuko ya bondeni; Nione kama mzabibu umechanua, Kama mikomamanga imetoa maua. 12 Kabla sijajua, roho yangu ilinileta Katikati ya magari ya wakuu wangu. 13 Rudi, rudi, Mshulami, Rudi, rudi, ili sisi tukutazame.

Wimbo Ulio Bora 7

1 Siti msharifu, jinsi zilivyo nzuri Hatua zako katika mitalawanda. Mapaja yako ya mviringo ni kama johari, Kazi ya mikono ya fundi mstadi; 2 Kitovu chako ni kama bilauri iliyoviringana, Na isikose divai iliyochanganyika; Tumbo lako ni mfano wa chungu ya ngano, Iliyozungukwa na ugo wa nyinyoro; 3 Maziwa yako mawili ni kama wana-paa wawili, Ambao ni mapacha ya paa; 4 Shingo yako ni kama huo mnara wa pembe; Macho yako kama viziwa vya Heshboni, Karibu na mlango wa Beth-rabi; Pua yako ni kama mnara wa Lebanoni, Unaoelekea Dameski; 5 Kichwa chako juu yako ni kama Karmeli, Na nywele za kichwa chako kama urujuani, Mfalme amenaswa na mashungu yake. 6 Jinsi yalivyo mazuri, yalivyo matamu, Mapenzi katikati ya anasa! 7 Kimo chako kimefanana na mtende, Na maziwa yako na vichala. 8 Nilisema, Nitapanda huo mtende, Na kuyashika makuti yake. Maziwa yako na yawe kama vichala vya mzabibu, Na harufu ya pumzi yako kama mapera; 9 Na kinywa chako kama divai iliyo bora, Kwa mpendwa wangu inashuka taratibu, Ikitiririka midomoni mwao walalao. 10 Mimi ni wake mpendwa wangu, Na shauku yake ni juu yangu. 11 Njoo, mpendwa wangu, twende mashambani, Tufanye maskani katika vijiji. 12 Twende mapema hata mashamba ya mizabibu, Tuone kama mzabihu umechanua, Na maua yake yamefunuka; Kama mikomamanga imetoa maua; Huko nitakupa pambaja zangu. 13 Mitunguja hutoa harufu yake; Juu ya milango yetu yako matunda mazuri, Mapya na ya kale, ya kila namna, Niliyokuwekea, mpendwa wangu.

Wimbo Ulio Bora 8

1 Laiti ungekuwa kama ndugu yangu, Aliyeyanyonya matiti ya mamangu! Kama ningekukuta huko nje, Ningekubusu, asinidharau mtu. 2 Ningekuongoza nyumbani mwa mamangu, Naye angenifundisha; Ningekunywesha divai iliyokolea,Divai mpya ya mkomamanga wangu. 3 Mkono wake wa kushoto ungekuwa chini ya kichwa changu, Nao wa kuume ungenikumbatia. 4 Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, Kwani kuyachochea mapenzi, au kuyaamsha, Hata yatakapoona vema? 5 Ni nani huyu apandaye kutoka nyikani, Akimtegemea mpendwa wake? Nalikuamsha chini ya huo mpera; Huko mama yako alikuonea utungu, Aliona utungu aliyekuzaa. 6 Nitie kama muhuri moyoni mwako, Kama muhuri juu ya mkono wako; Kwa maana upendo una nguvu kama mauti, Na wivu ni mkali kama ahera. Mwako wake ni mwako wa moto, Na miali yake ni miali ya Yahu. 7 Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo, Wala mito haiwezi kuuzamisha; Kama mtu angetoa badala ya upendo Mali yote ya nyumbani mwake, Angedharauliwa kabisa. 8 Kwetu sisi tuna umbu mdogo, Wala hana maziwa; Tumfanyieje umbu letu, Siku atakapoposwa? 9 Kama akiwa tu ukuta, Tumjengee buruji za fedha; Na kama akiwa ni mlango, Tumhifadhi kwa mbao za mierezi. 10 Mimi nalikuwa ukuta, Na maziwa yangu kama minara; Ndipo nikawa machoni pake Kama mtu aliyeipata amani. 11 Sulemani alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-hamomi Akawakodisha walinzi hilo shamba lake la mizabibu; Kila mtu atoe vipande elfu vya fedha kwa matunda yake. 12 Shamba langu la mizabibu, lililo langu mimi, li mbele yangu. Basi, Sulemani, wewe uwe na elfu zako, Na hao wayalindao matunda yake wapewe mia mbili. 13 Wewe ukaaye bustanini, Hao rafiki huisikiliza sauti yako; Unisikizishe mimi. 14 Ukimbie, mpendwa wangu, Nawe uwe kama paa, au ayala, Juu ya milima ya manukato.

Isaya 1

1 Haya ni maono ya Isaya, mwana wa Amozi, aliyoyaona katika habari za Yuda na Yerusalemu, siku za Uzia na Yothamu na Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda. 2 Sikieni, enyi mbingu, tega sikio, Ee nchi, kwa maana Bwana amenena; Nimewalisha watoto na kuwalea, nao wameniasi. 3 Ng'ombe amjua bwana wake, Na punda ajua kibanda cha bwana wake; Bali Israeli hajui, watu wangu hawafikiri. 4 Ole wake, taifa lenye dhambi, watu wanaochukua mzigo wa uovu, wazao wa watenda mabaya, watoto wanaoharibu; wamemwacha Bwana, wamemdharau yeye aliye Mtakatifu wa Israeli, wamefarakana naye na kurudi nyuma. 5 Mbona mnataka kupigwa hata sasa, hata mkazidi kuasi? Kichwa chote ni kigonjwa, moyo wote umezimia. 6 Tangu wayo wa mguu hata kichwani hamna uzima ndani yake; bali jeraha na machubuko na vidonda vitokavyo usaha; havikufungwa, havikuzongwa-zongwa, wala havikulainishwa kwa mafuta. 7 Nchi yenu ni ukiwa; miji yenu imeteketezwa kwa moto; nchi yenu, wageni wameila mbele ya macho yenu; nayo ni ukiwa, kana kwamba imeangamizwa na wageni. 8 Na binti Sayuni ameachwa kama kibanda katika shamba la mizabibu, kama kipenu katika shamba la matango, kama mji uliohusuriwa. 9 Kama Bwana wa majeshi asingalituachia mabaki machache sana, tungalikuwa kama Sodoma, tungalifanana na Gomora. 10 Lisikieni neno la Bwana, enyi waamuzi wa Sodoma; tegeni masikio msikie sheria ya Mungu wetu, enyi watu wa Gomora. 11 Huu wingi wa sadaka zenu mnazonitolea una faida gani? Asema Bwana. Nimejaa mafuta ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng'ombe wala ya wana-kondoo wala ya mbuzi waume. 12 Mjapo ili kuonekana mbele zangu, ni nani aliyetaka neno hili mikononi mwenu, kuzikanyaga nyua zangu? 13 Msilete tena matoleo ya ubatili; uvumba ni chukizo kwangu; mwezi mpya na sabato, kuita makutano; siyawezi maovu hayo na makutano ya ibada. 14 Sikukuu zenu za mwezi mpya na karamu zenu zilizoamriwa, nafsi yangu yazichukia; mambo hayo yanilemea; nimechoka kuyachukua. 15 Nanyi mkunjuapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, mwombapo maombi mengi, sitasikia; mikono yenu imejaa damu. 16 Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; 17 jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane. 18 Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu. 19 Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi; 20 bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha Bwana kimenena haya. 21 Mji huu uliokuwa mwaminifu umekuwaje kahaba! Yeye aliyejaa hukumu ya haki; haki ilikaa ndani yake, bali sasa wauaji! 22 Fedha yako imekuwa takataka, divai yako imechanganywa na maji. 23 Wakuu wako ni waasi, na rafiki za wevi; kila mtu hupenda rushwa, hufuata malipo; hawampatii yatima haki yake, wala maneno ya mjane hayawawasilii. 24 Kwa hiyo, asema Bwana, Bwana wa majeshi, Mwenye enzi, wa Israeli, Nitapata faraja kwa hao wanipingao, nitatwaa kisasi kwa adui zangu; 25 nami nitakuelekezea wewe mkono wangu, na kukutakasa takataka zako kabisa, na kukuondolea bati lako lote; 26 nami nitarejeza upya waamuzi wako kama walivyokuwa hapo kwanza, na washauri wako kama hapo mwanzo; baada ya hayo utaitwa, Mji wa haki, mji mwaminifu. 27 Sayuni itakombolewa kwa hukumu, na waongofu wake kwa haki. 28 Lakini kuharibika kwao wakosao nao wenye dhambi kutatokea wakati mmoja, nao wamwachao Bwana watateketezwa. 29 Kwa maana watatahayarika kwa sababu ya mialoni mliyoitamani, nanyi mtaaibishwa kwa sababu ya bustani mlizozichagua. 30 Maana mtakuwa kama mwaloni ambao majani yake yakauka, na kama bustani isiyo na maji. 31 Na mtu hodari atakuwa kama makumbi, na kazi yake kama cheche ya moto; nao watawaka pamoja, wala hapana atakayewazima.

Isaya 2

1 Hili ni neno aliloliona Isaya mwana wa Amozi katika habari za Yuda na Yerusalemu. 2 Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya Bwana utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. 3 Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana katika Yerusalemu. 4 Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. 5 Enyi wa nyumba ya Israeli, njoni, twende katika nuru ya Bwana. 6 Maana wewe umewaacha watu wako, nyumba ya Israeli, kwa sababu wamejaa kawaida za mashariki, nao ni wapiga ramli kama Wafilisti, na wanapana mikono na wana wa wageni. 7 Tena nchi yao imejaa fedha na dhahabu, wala hapana mwisho wa hazina zao; tena nchi yao imejaa farasi, wala hapana mwisho wa magari yao. 8 Tena nchi yao imejaa sanamu; huabudu kazi ya mikono yao, vitu vilivyofanywa kwa vidole vyao wenyewe. 9 Mtu mnyonge huinama, na mtu mkubwa hujidhili; kwa hiyo usiwasamehe. 10 Ingia ndani ya jabali; ukajifiche mavumbini mbele za utisho wa Bwana, mbele za utukufu wa enzi yake. 11 Macho ya mwanadamu yaliyoinuka yatashushwa chini, na kiburi cha mwanadamu kitainamishwa, naye Bwana, yeye peke yake, atatukuzwa siku hiyo. 12 Kwa maana kutakuwa siku ya Bwana wa majeshi juu ya watu wote wenye kiburi na majivuno, na juu ya yote yaliyoinuka; nayo yatashushwa chini. 13 Na juu ya mierezi yote ya Lebanoni iliyo mirefu na kuinuka, na juu ya mialoni yote ya Bashani; 14 na juu ya milima mirefu yote, na juu ya vilima vyote vilivyoinuka; 15 na juu ya kila mnara mrefu, na juu ya kila ukuta ulio na boma; 16 na juu ya merikebu zote za Tarshishi, na juu ya kila taswira ipendezayo. 17 Na majivuno ya mwanadamu yatainamishwa, na kiburi cha watu kitashushwa; naye Bwana, yeye peke yake, atatukuzwa siku hiyo. 18 Nazo sanamu zitatoweka kabisa. 19 Na watu wataingia ndani ya pango za majabali, na ndani ya mashimo ya nchi, mbele za utisho wa Bwana na utukufu wa enzi yake, atakapoondoka ili aitetemeshe mno dunia. 20 Siku hiyo kila mtu atazitupilia mbali sanamu zake za fedha, na sanamu zake za dhahabu, walizojifanyia ili kuziabudu, kwa fuko na popo; 21 ili aingie ndani ya pango za majabali, na ndani ya tundu za miamba iliyopasuka, mbele za utisho wa Bwana na utukufu wa enzi yake, atakapoondoka ili aitetemeshe mno dunia. 22 Mwacheni mwanadamu ambaye pumzi yake i katika mianzi ya pua yake; kwa maana hudhaniwaje kuwa ni kitu?

Isaya 3

1 Kwa maana, tazama, Bwana, Bwana wa majeshi, awaondolea Yerusalemu na Yuda egemeo na tegemeo; tegemeo lote la chakula na tegemeo lote la maji; 2 mtu hodari na mtu wa vita; mwamuzi na nabii; mpiga ramli na mzee; 3 jemadari aliye juu ya watu hamsini, na mtu mstahifu, na mshauri, na fundi aliye mstadi, na mganga ajuaye uganga sana. 4 Nami nitawapa watoto kuwamiliki, na watoto wachanga kuwatawala. 5 Nao watu wataonewa, kila mtu na mwenziwe, na kila mtu na jirani yake; mtoto atajivuna mbele ya mzee, na mtu mnyonge mbele ya mtu mwenye heshima. 6 Mtu atakapomshika ndugu yake ndani ya nyumba ya baba yake, akisema, Wewe una nguo, ututawale wewe; na mahali hapa palipobomoka pawe chini ya mkono wako; 7 basi, siku ile atainua sauti yake, akisema, Mimi sitakuwa mponya watu; kwa maana ndani ya nyumba yangu hamna chakula wala mavazi; wala hamtanifanya kuwa mtawala juu ya watu hawa. 8 Kwa maana Yerusalemu umebomolewa na Yuda wameanguka, kwa sababu ulimi wao na matendo yao ni kinyume cha Bwana, hata wayachukize macho ya utukufu wake. 9 Kuonekana kwa nyuso zao kwashuhudia juu yao, wafunua dhambi yao kama Sodoma, hawaifichi. Ole wa nafsi zao, kwa maana wamejilipa nafsi zao uovu. 10 Waambieni wenye haki ya kuwa watakuwa heri, kwa maana watakula matunda ya matendo yao 11 Ole wake mtu mbaya; shari itakuwa kwake, kwa maana atapewa ijara ya mikono yake. 12 Katika habari za watu wangu, watoto ndio wanaowaonea, na wanawake ndio wanaowatawala. Enyi watu wangu, wakuongozao wakukosesha, waiharibu njia ya mapito yako. 13 Bwana asimama ili atete, asimama ili awahukumu watu. 14 Bwana ataingia katika kuwahukumu wazee wa watu wake na wakuu wao; Ninyi ndinyi mliokula shamba la mizabibu; vitu mlivyowateka maskini vi ndani ya nyumba zenu. 15 Ni nini maana yake, ninyi kuwaonea watu wangu, na kuseta nyuso za maskini? Asema Bwana, Bwana wa majeshi. 16 Bwana akasema tena, Kwa sababu binti za Sayuni wana kiburi, na kuenenda na shingo zilizonyoshwa, na macho ya kutamani, wakienenda kwa hatua za madaha, na kuliza njuga kwa miguu yao; 17 Basi, kwa hiyo, Bwana atawapiga binti za Sayuni kwa pele za utosini, na Bwana ataifunua aibu yao. 18 Siku hiyo Bwana atawaondolea uzuri wa njuga zao, na kaya zao; 19 na pete za masikio, na vikuku, na taji zao; 20 na dusumali, na mafurungu, na vitambi, na vibweta vya marashi, na matalasimu; 21 na pete, na azama, 22 na mavazi ya sikukuu, na debwani; na shali, na vifuko; 23 na vioo vidogo, na kitani nzuri, na vilemba, na utaji. 24 Hata itakuwa ya kuwa badala ya manukato mazuri kutakuwa uvundo, na badala ya mishipi, kamba; na badala ya nywele zilizosukwa vizuri, upaa; na badala ya kisibau, mavazi ya kigunia; na kutiwa alama mwilini kwa moto badala ya uzuri. 25 Watu wako waume wataanguka kwa upanga, na mashujaa wako vitani. 26 Na malango yake yatalia na kuomboleza, naye atakuwa ukiwa, atakaa chini.

Isaya 4

1 Na siku hiyo wanawake saba watamshika mtu mume mmoja wakisema, Tutakula chakula chetu, na kuvaa nguo zetu wenyewe, lakini tuitwe tu kwa jina lako; utuondolee aibu yetu. 2 Siku hiyo chipukizi la Bwana litakuwa zuri, lenye utukufu, na matunda ya nchi yatakuwa mema sana, na kupendeza, kwa ajili ya Waisraeli wale waliookoka. 3 Tena itakuwa ya kwamba yeye aliyebaki katika Sayuni, na yeye aliyeachwa ndani ya Yerusalemu, ataitwa mtakatifu; yaani, kila mmoja aliyeandikwa miongoni mwa hao walio hai ndani ya Yerusalemu; 4 hapo Bwana atakapokuwa ameuosha uchafu wa hao binti za Sayuni na kuisafisha damu ya Yerusalemu kati yake, kwa roho ya hukumu na kwa roho ya kuteketeza. 5 Tena juu ya makao yote ya mlima Sayuni, na juu ya makusanyiko yake, Bwana ataumba wingu na moshi wakati wa mchana, na mwangaza wa miali ya moto wakati wa usiku; kwa maana juu ya utukufu wote itatandazwa sitara. 6 Kisha kutakuwa na hema kuwa uvuli wakati wa mchana kwa sababu ya hari, na kuwa mahali pa kukimbilia na kujificha wakati wa tufani na mvua.

Isaya 5

1 Na nimwimbie mpenzi wangu wimbo wa mpenzi wangu katika habari za shamba lake la mizabibu. Mpenzi wangu alikuwa na shamba la mizabibu, Kilimani penye kuzaa sana; 2 Akafanya handaki kulizunguka pande zote, Akatoa mawe yake, Akapanda ndani yake mzabibu ulio mzuri, Akajenga mnara katikati yake, Akachimba shinikizo ndani yake; Akatumaini ya kuwa utazaa zabibu, Nao ukazaa zabibu-mwitu. 3 Na sasa, enyi wenyeji wa Yerusalemu, nanyi watu wa Yuda, amueni, nawasihi, kati ya mimi na shamba langu la mizabibu. 4 Je! Ni kazi gani iliyoweza kutendeka ndani ya shamba langu la mizabibu nisiyoitenda? Basi, nilipotumaini ya kuwa litazaa zabibu, mbona lilizaa zabibu-mwitu? 5 Haya basi, sasa nitawaambieni nitakalolitenda shamba langu la mizabibu; nitaondoa kitalu chake, nalo litaliwa; nitabomoa ukuta wake, nalo litakanyagwa; 6 nami nitaliharibu; wala halitapogolewa wala kulimwa, bali litamea mbigili na miiba; nami nitayaamuru mawingu yasinyeshe mvua juu yake. 7 Kwa maana shamba la mizabibu la Bwana wa majeshi ndilo nyumba ya Israeli, na watu wa Yuda ni mche wake wa kupendeza; akatumaini kuona hukumu ya haki, na kumbe! Aliona dhuluma; alitumaini kuona haki, na kumbe! Alisikia kilio. 8 Ole wao waongezao nyumba baada ya nyumba, na kuweka shamba karibu na shamba, hata hapana nafasi tena, nanyi hamna budi kukaa peke yenu kati ya nchi! 9 Bwana wa majeshi asema katika masikio yangu, Hakika majumba mengi yatakuwa ukiwa, naam, majumba makubwa, mazuri, yatakuwa hayana watu. 10 Kwa maana shamba la mizabibu la eka kumi litatoa bathi moja tu, na homeri ya mbegu itatoa efa tu. 11 Ole wao waamkao asubuhi na mapema, wapate kufuata kileo; wakishinda sana hata usiku wa manane mpaka mvinyo imewaka kama moto ndani yao! 12 Na kinubi, na zeze, na matari, na filimbi, na mvinyo, zote ziko katika karamu zao; lakini hawaiangalii kazi ya Bwana wala kuyafikiri matendo ya mikono yake. 13 Kwa sababu hiyo watu wangu wamechukuliwa mateka, kwa kukosa kuwa na maarifa; na watu wao wenye cheo wana njaa, na wengi wao waona kiu sana. 14 Kwa hiyo kuzimu kumeongeza tamaa yake, kumefunua kinywa chake bila kiasi; na utukufu wao, na wingi wao, na ghasia yao, naye pia afurahiye miongoni mwao, hushuka na kuingia humo. 15 Na mtu mnyonge ainamishwa, na mtu mkubwa amedhilika, na macho yao walioinuka hunyenyekezwa, 16 bali Bwana wa majeshi ametukuzwa katika hukumu, na Mungu aliye Mtakatifu ametakaswa katika haki. 17 Ndipo wana-kondoo watakapolisha kama katika malisho yao wenyewe, na mahali pao waliowanda, palipoachwa ukiwa, wageni watakula. 18 Ole wao wavutao uovu kwa kamba za ubatili, na dhambi kama kwa kamba za gari! 19 Wasema, Na afanye haraka, aihimize kazi yake, tupate kuiona; na likaribie shauri lake aliye Mtakatifu wa Israeli, tupate kuliona. 20 Ole wao wasemao kwamba uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu; watiao giza badala ya nuru, na nuru badala ya giza; watiao uchungu badala ya utamu, na utamu badala ya uchungu! 21 Ole wao walio wenye hekima katika macho yao wenyewe, na wenye busara katika fikira zao wenyewe! 22 Ole wao walio hodari kunywa kileo chenye nguvu, watu waume wenye nguvu kuchanganya vileo; 23 wampao haki mwenye uovu, ili wapewe ijara, na kumwondolea mwenye haki haki yake! 24 Kwa hiyo kama vile mwali wa moto uteketezavyo mabua makavu, na kama manyasi makavu yaangukavyo katika mwali wa moto; kadhalika shina lao litakuwa kama ubovu, na ua lao litapeperushwa juu kama mavumbi; kwa sababu wameikataa sheria ya Bwana wa majeshi, na kulidharau neno lake aliye Mtakatifu wa Israeli. 25 Kwa sababu hiyo hasira ya Bwana imewaka juu ya watu wake, naye amenyosha mkono wake juu yao; akawapiga, navyo vilima vilitetemeka, na mizoga yao ilikuwa kama takataka katika njia kuu. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa. 26 Naye atawatwekea bendera mataifa toka mbali, Naye atawapigia miunzi tokea mwisho wa nchi; Na tazama, watakuja mbio mbio upesi sana. 27 Miongoni mwao hakuna achokaye wala kukwaa; Hakuna asinziaye wala kulala usingizi; Wala mshipi wa viuno vyao hautalegea. Wala ukanda wa viatu vyao hautakatika; 28 Mishale yao ni mikali, na pindi zao zote zimepindika; Kwato za farasi zao zitahesabika kama gumegume; Na gurudumu zao kama kisulisuli; 29 Ngurumo yao itakuwa kama ya simba; Watanguruma kama wana-simba; Naam, watanguruma na kukamata mateka, Na kuyachukua na kwenda zao salama, Wala hakuna mtu atakayeokoa. 30 Nao watanguruma juu yao siku hiyo Kama ngurumo ya bahari; Na mtu akiitazama nchi, ataona giza na dhiki Nayo nuru imetiwa giza katika mawingu yake.

Isaya 6

1 Katika mwaka ule aliokufa mfalme Uzia nalimwona Bwana ameketi katika kiti cha enzi, kilicho juu sana na kuinuliwa sana, na pindo za vazi lake zikalijaza hekalu. 2 Juu yake walisimama maserafi; kila mmoja alikuwa na mabawa sita; kwa mawili alifunika uso wake, na kwa mawili alifunika miguu yake, na kwa mawili aliruka. 3 Wakaitana, kila mmoja na mwenzake, wakisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, ni Bwana wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake. 4 Na misingi ya vizingiti ikatikisika kwa sababu ya sauti yake aliyelia, nayo nyumba ikajaa moshi. 5 Ndipo niliposema, Ole wangu! Kwa maana nimepotea; kwa sababu mimi ni mtu mwenye midomo michafu, nami ninakaa kati ya watu wenye midomo michafu; na macho yangu yamemwona Mfalme, Bwana wa majeshi. 6 Kisha mmoja wa maserafi wale akaruka akanikaribia; naye alikuwa na kaa la moto mkononi mwake, ambalo alikuwa amelitwaa kwa makoleo toka juu ya madhabahu; 7 akanigusa kinywa changu kwa kaa hilo, akaniambia, Tazama, hili limekugusa midomo yako, na uovu wako umeondolewa, na dhambi yako imefunikwa. 8 Kisha nikaisikia sauti ya Bwana, akisema, Nimtume nani, naye ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu? Ndipo niliposema, Mimi hapa, nitume mimi. 9 Naye akaniambia, Enenda, ukawaambie watu hawa, Fulizeni kusikia, lakini msifahamu; fulizeni kutazama, lakini msione. 10 Uunoneshe moyo wa watu hawa, ukayatie uzito masikio yao, ukayafumbe macho yao; wasije wakaona kwa macho yao, na kusikia kwa masikio yao, na kufahamu kwa mioyo yao, na kurejea na kuponywa. 11 Ndipo nilipouliza, Ee Bwana, hata lini? Naye akanijibu, Hata miji itakapokuwa ukiwa, haina wenyeji, na nyumba zitakapokuwa hazina watu, na nchi hii itakapokuwa ganjo kabisa; 12 hata Bwana atakapowahamisha watu waende mbali sana, na mahame yatakapokuwa mengi ndani ya nchi. 13 Na ijapokuwa imebaki sehemu moja katika sehemu kumi ndani yake, italiwa hii nayo; kama mvinje na kama mwaloni, ambao shina lake limebaki, ingawa imekatwa; kadhalika mbegu takatifu ndiyo shina lake.

Isaya 7

1 Hata ikawa katika siku za Ahazi, mwana wa Yothamu, mwana wa Uzia, mfalme wa Yuda, Resini, mfalme wa Shamu, na Peka, mwana wa Remalia, mfalme wa Israeli, wakapanda wakaenda Yerusalemu ili kupigana nao, lakini hawakuweza kuushinda. 2 Kisha watu wa nyumba ya Daudi wakaambiwa kwamba Shamu wamefanya mapatano na Efraimu. Na moyo wake ukataharuki, na moyo wa watu wake, kama miti ya mwituni itikiswavyo na upepo. 3 Basi Bwana akamwambia Isaya, Haya, toka, umlaki Ahazi, wewe na Shear-yashubu mwana wako, huko mwisho wa mfereji wa birika la juu, katika njia kuu ya uwanja wa dobi; 4 ukamwambie, Angalia, ukatulie; usiogope wala usife moyo, kwa sababu ya mikia hii miwili ya vinga hivi vitokavyo moshi; kwa sababu ya hasira kali ya Resini na Shamu, na mwana wa Remalia. 5 Kwa kuwa Shamu amekusudia mabaya juu yako, pamoja na Efraimu na mwana wa Remalia, wakisema, 6 Haya, na tupande ili kupigana na Yuda na kuwasumbua, tukabomoe mahali tupate kuingia, na kummilikisha mfalme ndani yake, huyo mwana wa Tabeeli. 7 Bwana MUNGU asema hivi, Neno hili halitasimama wala halitakuwa. 8 Kwa maana kichwa cha Shamu ni Dameski, na kichwa cha Dameski ni Resini; na katika muda wa miaka sitini na mitano Efraimu atavunjika vipande vipande, asiwe kabila ya watu tena; 9 tena kichwa cha Efraimu ni Samaria, na kichwa cha Samaria ni mwana wa Remalia. Kwamba hamtaki kusadiki, bila shaka hamtathibitika. 10 Tena Bwana akasema na Ahazi akinena, 11 Jitakie ishara ya Bwana, Mungu wako; itake katika mahali palipo chini sana, au katika mahali palipo juu sana. 12 Lakini Ahazi akasema, Sitaitaka, wala sitamjaribu Bwana. 13 Naye akasema, Sikilizeni sasa, enyi nyumba ya Daudi; Je! Ni neno dogo kwenu kuwachosha wanadamu, hata mkataka kumchosha Mungu wangu pia? 14 Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli. 15 Siagi na asali atakula, wakati ajuapo kuyakataa mabaya na kuyachagua mema. 16 Kwa maana kabla mtoto huyo hajajua kuyakataa mabaya na kuyachagua mema, nchi ile, ambayo wewe unawachukia wafalme wake wawili, itaachwa ukiwa. 17 Bwana ataleta juu yako, na juu ya watu wako, na juu ya nyumba ya baba yako, siku zisizokuja bado, tangu siku ile aliyoondoka Efraimu kutoka katika Yuda; yaani, mfalme wa Ashuru. 18 Tena itakuwa katika siku hiyo Bwana atampigia kelele inzi aliye katika pande za mwisho za mito ya Misri, na nyuki aliye katika nchi ya Ashuru 19 Nao watakuja na kutulia katika mabonde yaliyo ukiwa, na katika pango za majabali, na juu ya michongoma yote, na juu ya malisho yote. 20 Katika siku hiyo Bwana atanyoa kichwa na malaika ya miguuni, kwa wembe ulioajiriwa pande za ng'ambo ya Mto, yaani, kwa mfalme wa Ashuru, nao utazimaliza ndevu nazo. 21 Katika siku hiyo itakuwa ya kwamba mtu atalisha ng'ombe mke mchanga na kondoo wake wawili; 22 kisha itakuwa, kwa sababu wanyama hao watatoa maziwa mengi, atakula siagi; kwa maana kila mtu aliyesalia katika nchi hii atakula siagi na asali. 23 Tena itakuwa katika siku hiyo kila mahali palipokuwa na mizabibu elfu, iliyopata fedha elfu, patakuwa mahali pa mbigili na miiba tu. 24 Mtu atakayekwenda huko atakwenda na mishale na upinde; kwa sababu nchi yote itakuwa ina mibigili na miiba. 25 Na vilima vyote vilivyolimwa kwa jembe, hutafika huko kwa sababu ya kuiogopa mibigili na miiba, lakini hapo patakuwa mahali pa kupeleka ng'ombe, mahali pa kukanyagwa na kondoo.

Isaya 8

1 Bwana akaniambia, Ujipatie ubao mkubwa ukaandike juu yake kwa kalamu ya binadamu, Kwa Maher-shalal-hash-bazi; 2 nami nitajipatia mashahidi waaminifu ili kuandika habari, yaani, Uria, kuhani, na Zekaria, mwana wa Yeberekia. 3 Nami nikamwendea huyo nabii mke, naye akapata mimba, akazaa mtoto mwanamume. Kisha Bwana akaniambia, Mwite jina lake Maher-shalal-hash-bazi. 4 Kwa maana kabla mtoto huyo hajapata kujua kusema, Baba yangu, na Mama yangu, hazina za Dameski na mateka ya Samaria yatachukuliwa mbele ya mfalme wa Ashuru. 5 Kisha Bwana akasema nami mara ya pili, akaniambia, 6 Kwa sababu watu hawa wameyakataa maji ya Shiloa yapitayo polepole, na kufurahi kwa ajili ya Resini na huyo mwana wa Remalia, 7 basi sasa angalia; Bwana aleta juu yao maji ya huo Mto, yenye nguvu, mengi sana, nayo ni mfalme wa Ashuru na utukufu wake wote; naye atakuja, na kupita juu ya mifereji yake yote, atafurika juu ya kingo zake zote; 8 naye atapita, atapita kwa kasi na kuingia Yuda; atafurika na kupita katikati, atafika hata shingoni; na kule kuyanyosha mabawa yake kutaujaza upana wa nchi yako, Ee Imanueli. 9 Fanyeni ghasia, enyi kabila za watu, Nanyi mtavunjwa vipande vipande; Tegeni masikio, ninyi nyote wa nchi zilizo mbali; Jikazeni viuno, nanyi mtavunjwa vipande vipande; Jikazeni viuno, nanyi mtavunjwa vipande vipande. 10 Fanyeni shauri pamoja, nalo litabatilika; Semeni neno, lakini halitasimama; Kwa maana Mungu yu pamoja nasi. 11 Maana Bwana aliniambia hivi, kwa mkono hodari, akanifundisha nisiende katika njia ya watu hawa, akisema, 12 Msiseme, Ni fitina, katika habari za mambo yote ambayo watu hawa watasema, Ni fitina; msihofu kwa hofu yao, wala msiogope. 13 Bwana wa majeshi ndiye mtakayemtakasa; na awe yeye hofu yenu, na awe yeye utisho wenu. 14 Naye atakuwa ni mahali patakatifu; bali ni jiwe la kujikwaza na mwamba wa kujikwaa kwa nyumba za Israeli zote mbili, na mtego na tanzi kwa wenyeji wa Yerusalemu. 15 Na wengi watajikwaa juu yake, na kuanguka na kuvunjika, na kunaswa na kukamatwa. 16 Ufunge huo ushuhuda, ukaitie muhuri sheria kati ya wanafunzi wangu. 17 Nami nitamngojea Bwana, awafichaye uso wake nyumba ya Yakobo, nami nitamtazamia. 18 Angalieni, mimi na watoto hawa niliopewa na Bwana tu ishara na ajabu katika Israeli, zitokazo kwa Bwana wa majeshi, yeye akaaye katika mlima Sayuni. 19 Na wakati watakapokuambia, Tafuta habari kwa watu wenye pepo na kwa wachawi; waliao kama ndege na kunong'ona; je! Haiwapasi watu kutafuta habari kwa Mungu wao? Je! Waende kwa watu waliokufa kwa ajili ya watu walio hai? 20 Na waende kwa sheria na ushuhuda; ikiwa hawasemi sawasawa na neno hili, bila shaka kwa hao hapana asubuhi. 21 Nao watapita katikati yake, wamedhikika sana na kuwa na njaa; na itakuwa watakapoona njaa, watalalamika na kuapa kwa mfalme wao, na kwa Mungu wao, na kuelekeza nyuso zao juu; 22 nao wataiangalia nchi, na, tazama, shida na giza; hapana changamko kwa sababu ya dhiki; nao watafukuzwa na kuingia katika giza kubwa.

Isaya 9

1 Lakini yeye aliyekuwa katika dhiki hatakosa changamko. Hapo kwanza aliiingiza nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali katika hali ya kudharauliwa, lakini zamani za mwisho ameifanya kuwa tukufu, karibu na njia ya bahari; ng'ambo ya Yordani, Galilaya ya mataifa. 2 Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza. 3 Umeliongeza taifa, umezidisha furaha yao; Wanafurahi mbele zako, Kama furaha ya wakati wa mavuno, Kama watu wafurahivyo wagawanyapo nyara. 4 Kwa maana umeivunja nira ya mzigo wake, na gongo la bega lake, na fimbo yake yeye aliyemwonea, kama katika siku ya Midiani. 5 Maana silaha zote za mtu mwenye silaha wakati wa mshindo, na mavazi yaliyofingirishwa katika damu, yatakuwa tayari kuteketezwa, yatakuwa kuni za kutiwa motoni. 6 Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. 7 Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo. 8 Bwana alimpelekea Yakobo neno, likamfikilia Israeli. 9 Nao watu wote watajua, yaani, Efraimu na yeye akaaye Samaria, wasemao kwa kiburi na kwa kujisifu nafsi zao, 10 Matofali yameanguka, lakini sisi tutajenga kwa mawe yaliyochongwa; mikuyu imekatwa lakini sisi tutaweka mierezi badala yake. 11 Kwa sababu hiyo Bwana atawainua adui wa Resini juu yake, naye atawachochea adui zake; 12 Waashuri upande wa mbele, na Wafilisti upande wa nyuma, nao watamla Israeli kwa kinywa kilicho wazi. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa. 13 Lakini watu hao hawakumwelekea yeye aliyewapiga, wala kumtafuta Bwana wa majeshi. 14 Kwa sababu hiyo Bwana atakata katika Israeli kichwa na mkia, kuti na nyasi, katika siku moja. 15 Mzee mwenye kuheshimiwa ndiye kichwa, na nabii afundishaye uongo ndiye mkia. 16 Kwa maana wawaongozao watu hawa ndio wawakoseshao, na hao walioongozwa na watu hao wameangamia. 17 Kwa sababu hiyo Bwana hatawafurahia vijana wao, wala hatawahurumia yatima zao wala wajane wao; maana kila mtu ni mnajisi, dhalimu, na kila ulimi hunena upumbavu. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa. 18 Kwa maana uovu huteketeza kama moto; huila mibigili na miiba, naam, huwaka katika vichaka vya mwitu, nao hupaa juu katika mawingu mazito ya moshi. 19 Kwa sababu ya hasira ya Bwana wa majeshi nchi hii inateketea kabisa; watu hawa nao ni kama kuni zitiwazo motoni; hapana mtu amhurumiaye ndugu yake. 20 Hupokonya upande wa mkono wa kuume, nao huona njaa! Hula upande wa mkono wa kushoto, wala hawashibi! Watakula kila mtu nyama ya mkono wake mwenyewe. 21 Manase anamla Efraimu, naye Efraimu anamla Manase; nao wawili pamoja watakuwa juu ya Yuda. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa.

Isaya 10

1 Ole wao wawekao amri zisizo za haki, na waandishi waandikao maneno ya ushupavu; 2 ili kumpotosha mhitaji asipate haki yake, na kuwanyang'anya maskini wa watu wangu haki yao; ili wajane wawe mateka yao, na kuwafanya yatima waliofiwa na baba zao kuwa mawindo yao! 3 Nanyi mtafanya nini siku ya kujiliwa, na wakati wa uangamivu, utakaokuja kutoka mbali sana? Je! Mtamkimbilia nani mpate msaada? Na utukufu wenu mtauacha wapi? 4 Watainama chini ya wafungwa tu, wataanguka chini yao waliouawa. Pamoja na hayo yote hasira yake haikugeukia mbali, lakini mkono wake umenyoshwa hata sasa. 5 Ole wake Ashuru! Fimbo ya hasira yangu, ambaye gongo lililo mkononi mwake ni ghadhabu yangu! 6 Nitamtuma juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya watu wa ghadhabu yangu, ateke nyara, na kuchukua mateka, na kuwakanyaga kama matope ya njiani. 7 Lakini hivyo sivyo akusudiavyo mwenyewe, wala sivyo moyo wake uwazavyo; maana katika moyo wake akusudia kuharibu, na kukatilia mbali mataifa, wala si mataifa machache. 8 Maana asema, Je! Wakuu wangu si wote wafalme? 9 Je! Kalno si kama Karkemishi? Hamathi si kama Arpadi? Samaria si kama Dameski? 10 Kama vile mkono wangu ulivyofikilia falme za sanamu, ambazo sanamu zao za kuchongwa zilikuwa bora kuliko sanamu za Yerusalemu na za Samaria; 11 je! Sitautenda Yerusalemu na sanamu zake vile vile kama nilivyoutenda Samaria na sanamu zake? 12 Basi, itakuwa, Bwana atakapokuwa ameitimiza kazi yake yote juu ya mlima Sayuni na juu ya Yerusalemu, nitayaadhibu matunda ya kiburi cha moyo wake mfalme wa Ashuru, na majivuno ya macho yake. 13 Kwa maana amesema, Kwa nguvu za mkono wangu nimetenda jambo hili, na kwa hekima yangu; maana mimi nina busara; nami nimeiondoa mipaka ya watu, nikaziteka akiba zao, nikawaangusha waketio juu ya viti vya enzi kama afanyavyo shujaa. 14 Na mkono wangu umezitoa mali za mataifa kama katika kioto cha ndege; na kama vile watu wakusanyavyo mayai yaliyoachwa, ndivyo nilivyokusanya dunia yote; wala hapana aliyetikisa bawa, wala kufumbua kinywa, wala kulia. 15 Je! Shoka lijisifu juu yake alitumiaye? Je! Msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? Ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti. 16 Kwa hiyo Bwana, Bwana wa majeshi, atawapelekea kukonda watu wake walionona; na badala ya utukufu wake kutawashwa kuteketea kama kuteketea kwa moto. 17 Na mwanga wa Israeli utakuwa ni moto, na Mtakatifu wake atakuwa mwali wa moto; nao utateketeza na kula mbigili zake na miiba yake katika siku moja. 18 Naye atauteketeza utukufu wa msitu wake, na wa shamba lake linalositawi, tangu nafsi hata nyama ya mwili, itakuwa kama vile afapo mtu aliye mgonjwa. 19 Na miti ya msitu wake itakayosalia itakuwa michache, hata mtoto ataweza kuihesabu. 20 Tena itakuwa katika siku hiyo mabaki ya Israeli, na hao waliopona wa nyumba ya Yakobo, hawatamtegemea tena yeye aliyewapiga, bali watamtegemea Bwana, Mtakatifu wa Israeli, kwa kweli. 21 Mabaki, nao ni mabaki ya Yakobo, watamrudia Mungu, aliye mwenye nguvu. 22 Maana watu wako, Ee Israeli, wajapokuwa wengi kama mchanga wa pwani, ni mabaki tu watakaorudi; kuangamiza kumekusudiwa, kunakofurika kwa haki. 23 Kwa maana Bwana, Bwana wa majeshi, atayatimiza maangamizo yaliyokusudiwa katika nchi yote. 24 Kwa hiyo Bwana, Bwana wa majeshi, asema hivi, Enyi watu wangu mkaao katika Sayuni, msiogope Ashuru, ingawa akupiga kwa fimbo, na kuliinua gongo lake juu yako, kwa namna ya Kimisri. 25 Maana bado kitambo kidogo tu ghadhabu itakoma, na hasira yangu itageukia kuwaangamiza. 26 Na Bwana wa majeshi ataamsha mjeledi juu yake, kama vile alivyopiga Midiani karibu na jabali la Orebu; na fimbo yake itakuwa juu ya bahari, naye ataiinua kwa namna ya Kimisri. 27 Tena itakuwa katika siku hiyo mzigo wake utaondoka begani mwako, na nira yake shingoni mwako, nayo nira itaharibiwa, kwa sababu ya kutiwa mafuta. 28 Amefika Ayathi; amepita kati ya Migroni; ameweka mizigo yake huko Mikmashi; 29 wamevuka kivuko; wamekwenda kulala katika Geba; Rama unatetemeka; Gibea wa Sauli umekimbia. 30 Piga kelele sana, Ee binti Galimu; sikiliza, Ee Laisha; ole wako, maskini Anathothi! 31 Madmena ni mkimbizi; wenyeji wa Gebimu wamejikusanya wakimbie; 32 siku hii ya leo atasimama huko Nobu; anatikisa mkono wake juu ya mlima wa binti Sayuni, mlima wa Yerusalemu. 33 Angalia, Bwana, Bwana wa majeshi, atayakata matawi kwa nguvu za kutisha; nao walio warefu wa kimo watakatwa; na hao walioinuka wataangushwa chini; 34 naye atavikata vichaka vya msitu kwa chuma; na Lebanoni utaanguka kwa mkono wake aliye mwenye uweza.

Isaya 11

1 Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda. 2 Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana; 3 na furaha yake itakuwa katika kumcha Bwana; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; 4 bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya. 5 Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia. 6 Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. 7 Ng'ombe na dubu watalisha pamoja; watoto wao watalala pamoja; na simba atakula majani kama ng'ombe. 8 Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira. 9 Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua Bwana, kama vile maji yanavyoifunika bahari. 10 Na itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye ambaye mataifa watamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu. 11 Na itakuwa katika siku hiyo, Bwana atapeleka mkono wake mara ya pili, ili ajipatie watu wake watakaosalia, kutoka Ashuru, na kutoka Misri, na kutoka Pathrosi, na kutoka Kushi, na kutoka Elamu, na kutoka Shinari, na kutoka Hamathi, na kutoka visiwa vya bahari. 12 Naye atawatwekea mataifa bendera, atawakutanisha watu wa Israeli waliotupwa, atawakusanya watu wa Yuda waliotawanyika, kutoka ncha nne za dunia. 13 Na wivu wa Efraimu utaondoka, na wale wanaomwudhi Yuda watakatiliwa mbali; Efraimu hatamhusudu Yuda, wala Yuda hatamwudhi Efraimu. 14 Nao watashuka, watalirukia bega la Wafilisti upande wa magharibi; nao pamoja watawateka wana wa mashariki; watanyosha mkono juu ya Edomu na Moabu; na wana wa Amoni watawatii. 15 Na Bwana atauangamiza kabisa ulimi wa bahari ya Misri; na kwa upepo wake uteketezao atatikisa mkono wake juu ya Mto, naye ataupiga, uwe vijito saba, na kuwavusha watu wenye viatu vikavu. 16 Itakuwako njia kuu kwa mabaki ya watu wake watakaobaki, watokao Ashuru, kama vile ilivyokuwako kwa Israeli, katika siku ile waliyotoka katika nchi ya Misri.

Isaya 12

1 Na katika siku hiyo utasema, Ee Bwana, nitakushukuru wewe; Kwa kuwa ijapokuwa ulinikasirikia, Hasira yako imegeukia mbali, Nawe unanifariji moyo. 2 Tazama, Mungu ndiye wokovu wangu; Nitatumaini wala sitaogopa; Maana Bwana YEHOVA ni nguvu zangu na wimbo wangu; Naye amekuwa wokovu wangu. 3 Basi, kwa furaha mtateka maji katika visima vya wokovu. 4 Na katika siku hiyo mtasema, Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake; Yatangazeni matendo yake kati ya mataifa, Litajeni jina lake kuwa limetukuka. 5 Mwimbieni Bwana; kwa kuwa ametenda makuu; Na yajulikane haya katika dunia yote. 6 Paza sauti, piga kelele, mwenyeji wa Sayuni; Maana Mtakatifu wa Israeli ni mkuu kati yako.

Isaya 13

1 Ufunuo juu ya Babeli; maono aliyoyaona Isaya, mwana wa Amozi. 2 Haya! Juu ya mlima usio na miti inueni bendera, wapazieni sauti zenu, wapungieni mkono, kwamba waingie katika malango ya wakuu. 3 Mimi mwenyewe nimewaamuru watu wangu waliowekwa wakfu kwangu, naam, nimewaita watu wangu walio hodari kwa ajili ya hasira yangu, watu wangu wenye kutakabari. 4 Kelele milimani kama kelele za watu wengi sana; kelele za falme za mataifa waliokutana pamoja; Bwana wa majeshi anapanga jeshi kwa vita; 5 watu waliotoka katika nchi iliyo mbali, tokea upande wa mwisho wa mbingu; naam, Bwana na silaha za ghadhabu yake, ili aiangamize nchi yote. 6 Pigeni kelele za hofu; maana siku ya Bwana i karibu; itanyesha kama maangamizi yatokayo kwa Mwenyezi Mungu. 7 Kwa sababu hiyo mikono yote italegea, na moyo wa kila mtu utayeyuka. 8 Nao watafadhaika; watashikwa na utungu na maumivu; watakuwa na utungu kama mwanamke aliye karibu na kuzaa; watakodoleana macho; nyuso zao zitakuwa ni nyuso za moto. 9 Tazama, siku ya Bwana inakuja, siku kali, ya hasira na ghadhabu kuu, ili iifanye nchi kuwa ukiwa, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake. 10 Maana nyota za mbinguni na matangamano havitatoa nuru yake; jua litatiwa giza wakati wa kucha kwake, na mwezi utaacha nuru yake isiangaze. 11 Nami nitaadhibu ulimwengu kwa sababu ya ubaya wake, na wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali; 12 nitafanya wanadamu kuadimika kuliko dhahabu safi, na watu kuliko dhahabu ya Ofiri. 13 Kwa hiyo nitazitetemesha mbingu, na dunia itatikiswa itoke katika mahali pake, kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana wa majeshi, na kwa sababu ya siku ya hasira yake kali. 14 Basi, itakuwa kama vile paa aliyetishwa, na kama kondoo wasio na mtu wa kuwakusanya; kila mtu atageukia watu wake; nao watakimbia, kila mtu aende nchi yake mwenyewe. 15 Kila mtu atakayeonekana atatumbuliwa, na kila mtu atakayepatikana ataanguka kwa upanga. 16 Na watoto wao wachanga watavunjwa-vunjwa mbele ya macho yao, nyumba zao zitatekwa nyara, na wake zao watatendwa jeuri. 17 Tazama, nitawaamsha Wamedi juu yao, ambao hawaoni fedha kuwa kitu, wala hawafurahii dhahabu. 18 Na nyuta zao zitawaangusha vijana; wala hawatahurumia mazao ya tumbo; jicho lao halitawahurumia watoto. 19 Na Babeli, huo utukufu wa falme, uzuri wa kiburi cha Wakaldayo, utakuwa kama Sodoma na Gomora hapo Mungu alipoiangamiza. 20 Hautakaliwa na watu tena kabisa, wala watu hawatakaa ndani yake tangu kizazi hata kizazi. Mwarabu hatapiga hema yake huko, wala wachungaji hawatalaza makundi yao huko. 21 Lakini huko watalala hayawani wakali wa nyikani; na nyumba zao zitajaa bundi; mbuni watakaa huko; na majini watacheza huko. 22 Na mbwa-mwitu watalia ndani ya ngome zake; na mbweha ndani ya majumba ya anasa; na wakati wake u karibu kufika, na siku zake hazitaongezeka.

Isaya 14

1 Maana Bwana atamhurumia Yakobo, atamchagua Israeli tena, naye atawaweka katika nchi yao wenyewe; na mgeni atajiunga nao, nao wataambatana na nyumba ya Yakobo. 2 Na hao mataifa watawatwaa na kuwaleta mpaka mahali pao wenyewe, na nyumba ya Israeli watawamiliki, na kuwafanya watumishi na wajakazi katika nchi ya Bwana; nao watawachukua hali ya kufungwa watu wale waliowafunga wao, nao watawamiliki watu wale waliowaonea. 3 Tena itakuwa katika siku ile, ambayo Bwana atakupa raha baada ya huzuni yako, na baada ya taabu yako, na baada ya utumishi ule mgumu uliotumikishwa; 4 utatunga mithali hii juu ya mfalme wa Babeli, na kusema, Jinsi alivyokoma mwenye kuonea; Jinsi ulivyokoma mji ule wenye jeuri! 5 Bwana amelivunja gongo la wabaya, Fimbo ya enzi yao wenye kutawala. 6 Yeye aliyewapiga mataifa kwa ghadhabu, Kwa mapigo yasiyokoma; Aliyewatawala mataifa kwa hasira, Ameadhibiwa asizuie mtu. 7 Dunia yote inastarehe na kutulia; Hata huanzilisha kuimba. 8 Naam, misunobari inakufurahia, Na mierezi ya Lebanoni, ikisema, Tokea wakati ulipolazwa chini wewe, Hapana mkata miti aliyetujia. 9 Kuzimu chini kumetaharuki kwa ajili yako, Ili kukulaki utakapokuja; Huwaamsha waliokufa kwa ajili yako, Naam, walio wakuu wote wa dunia; Huwainua wafalme wote wa mataifa, Watoke katika viti vyao vya enzi. 10 Hao wote watajibu na kukuambia, Je! Wewe nawe umekuwa dhaifu kama sisi! Wewe nawe umekuwa kama sisi! 11 Fahari yako imeshushwa hata kuzimu, Na sauti ya vinanda vyako; Funza wametandazwa chini yako, Na vidudu vinakufunika. 12 Jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni, Ewe nyota ya alfajiri, mwana wa asubuhi! Jinsi ulivyokatwa kabisa, Ewe uliyewaangusha mataifa! 13 Nawe ulisema moyoni mwako, Nitapanda mpaka mbinguni, Nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, Katika pande za mwisho za kaskazini. 14 Nitapaa kupita vimo vya mawingu, Nitafanana na yeye Aliye juu. 15 Lakini utashushwa mpaka kuzimu; Mpaka pande za mwisho za shimo. 16 Wao wakuonao watakukazia macho, Watakuangalia sana, wakisema, Je! Huyu ndiye aliyeitetemesha dunia, Huyu ndiye aliyetikisa falme; 17 Aliyeufanya ulimwengu ukiwa, akaipindua miji yake; Asiyewafungua wafungwa wake waende kwao? 18 Wafalme wote wa mataifa wamezikwa wote kwa heshima, Kila mmoja ndani ya nyumba yake mwenyewe; 19 Bali wewe umetupwa mbali na kaburi lako, Kama chipukizi lililochukiza kabisa; Kama vazi la wale waliouawa, Wale waliochomwa kwa upanga, Wale washukao mpaka misingi ya shimo; Kama mzoga uliokanyagwa chini ya miguu. 20 Hutaungamanishwa pamoja nao katika mazishi, Kwa maana umeiharibu nchi yako, Umewaua watu wako; Kizazi chao watendao uovu hakitatajwa milele. 21 Fanyeni tayari machinjo kwa watoto wake. Kwa sababu ya uovu wa baba zao; Wasije wakainuka na kuitamalaki nchi, Na kuujaza miji uso wa ulimwengu. 22 Nami nitainuka, nishindane nao; asema Bwana wa majeshi; na katika Babeli nitang'oa jina na mabaki, mwana na mjukuu; asema Bwana. 23 Tena nitaifanya hiyo nchi kuwa makao ya nungu, na maziwa ya maji; nami nitaifagilia mbali kwa ufagio wa uharibifu; asema Bwana wa majeshi. 24 Bwana wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile vilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea; 25 kwamba nitamvunja huyo Mwashuri vipande vipande katika nchi yangu, na juu ya mlima wangu nitamkanyaga chini ya miguu yangu; ndipo nira yake iliyo juu yao itakapoondoka, na mzigo wake utatoka mabegani mwao. 26 Hilo ndilo kusudi lililokusudiwa duniani mwote, na huo ndio mkono ulionyoshwa juu ya mataifa yote. 27 Maana Bwana wa majeshi amekusudia, naye ni nani atakayelibatili? Na mkono wake ulionyoshwa, ni nani atakayeugeuza nyuma? 28 Ufunuo huu ulikuja mwaka ule alipokufa mfalme Ahazi. 29 Usifurahi, Ee Ufilisti, pia wote, Kwa sababu fimbo ile iliyokupiga imevunjika; Maana katika shina la nyoka atatoka fira, Na uzao wake ni joka la moto arukaye 30 Nao walio maskini kabisa watakula, Na wahitaji watajilaza salama; Nami nitatia shina lako kwa njaa, Na mabaki yako watauawa. 31 Piga yowe, Ee lango; lia, Ee mji; Ee Ufilisti, pia wote, umeyeyuka kabisa; Maana moshi unakuja toka kaskazini, Wala hakuna atakayechelewa katika majeshi yake. 32 Wajumbe wa taifa hilo waletewe jibu gani? Ya kuwa Bwana ameiweka misingi ya Sayuni, na ndani yake wale walioonewa katika watu wake wataona kimbilio.

Isaya 15

1 Ufunuo juu ya Moabu. Maana katika usiku mmoja Ari wa Moabu umeharibiwa kabisa na kuangamizwa; maana katika usiku mmoja Kiri wa Moabu umeharibiwa kabisa na kuangamizwa. 2 Wanapanda juu hata Bayithi na Diboni, mpaka mahali palipo juu ili walie; juu ya Nebo na juu ya Medeba Wamoabi wanalia; Wana upaa juu ya vichwa vyao vyote; kila ndevu zimenyolewa. 3 Wanajivika nguo za magunia katika njia kuu zao; juu ya dari zao, na katika mitaa yao, kila mtu analia, anamwaga machozi. 4 Heshboni analia na Eleale; mpaka Yahasa sauti ya kulia kwao inasikiwa; hata watu wa Moabu waliovaa silaha wanapiga kelele sana kwa sababu hiyo; nafsi yake inatetemeka ndani yake. 5 Moyo wangu unamlilia Moabu; wakuu wake wanakimbilia Soari kama ndama wa miaka mitatu; kwa maana wanapanda mbavu za Luhithi wakilia; maana katika njia iendayo hata Horonaimu wanapaliza sauti ya kukata tamaa. 6 Kwa maana maji ya Nimrimu yamekuwa mahali palipoharibika, kwa kuwa majani yamekauka, miche imenyauka, majani mabichi yamekoma. 7 Kwa hiyo vitu walivyojipatia tele, na akiba yao, wanavichukua hata kijito cha mierebi. 8 Maana kilio hicho kimezunguka mipaka ya Moabu, malalamiko yao yamefika hata Eglaimu, na malalamiko yao hata Beer-Elimu. 9 Maana maji ya Dimoni yamejaa damu; maana ninaweka tayari msiba mpya juu ya Dimoni, simba juu ya watu wa Moabu waliokimbia, na juu ya mabaki yao.

Isaya 16

1 Pelekeni wana-kondoo, kodi yake aitawalaye nchi toka Sela kuelekea jangwani, mpaka mlima wa binti Sayuni. 2 Na binti za Moabu watakuwa kama ndege warukao huko na huko, kama kioto cha ndege waliotiwa hofu, kwenye vivuko vya Arnoni. 3 Lete shauri; kata neno; fanya kivuli chako kuwa kama usiku kati ya mchana; wafiche waliofukuzwa; usiwachongee waliopotea. 4 Watu wangu waliofukuzwa waache wakae pamoja nawe; katika habari za Moabu, uwe sitara kwake mbele ya uso wake anayeharibu; maana yeye atozaye kwa nguvu amekoma; afanyaye ukiwa ametoweka; waliokanyaga watu wametoka katika nchi. 5 Na kiti cha enzi kitafanywa imara kwa rehema; na mmoja ataketi juu yake katika kweli, katika hema ya Daudi; akifanya hukumu, akitaka sana yaliyo haki, mwepesi wa kutenda haki. 6 Tumesikia habari za kiburi cha Moabu, ya kwamba ni mwenye kiburi kingi; habari za majivuno yake, na kiburi chake, na ghadhabu yake; majivuno yake si kitu. 7 Kwa sababu hiyo Moabu atalia kwa ajili ya Moabu, kila mmoja atalia, maana mtaiombolezea mikate ya zabibu ya Kir-Haresethi, mkipigwa sana. 8 Maana makonde ya Heshboni yamenyauka, na mzabibu wa Sibma; mabwana wa mataifa wameyavunja matawi yake mateule; yamefika hata Yazeri, yalitanga-tanga hata nyikani; matawi yake yalitapakaa, yaliivuka bahari. 9 Basi, naililia mizabibu ya Sibma kwa kilio cha Yazeri, nitawanyeshea machozi yangu, Ee Heshboni na Eleale, kwa kuwa kelele za vita zimeyaangukia mavuno ya matunda yako, na mavuno ya mizabibu yako. 10 Na furaha imeondolewa, na shangwe toka mashamba yaliyozaa sana; hapana kuimba katika mashamba ya mizabibu, wala sauti za furaha; akanyagaye hakanyagi divai katika mashinikizo; nimeikomesha sauti ya furaha yake akanyagaye. 11 Kwa sababu hiyo mtima wangu unamlilia Moabu kama kinubi, na matumbo yangu kwa ajili ya Kir-Heresi. 12 Tena itakuwa, Moabu akionekana, na kujichosha kwa kulia juu ya mahali pa juu, na kuingia katika patakatifu pake aombe, hatapata kushinda. 13 Hilo ndilo neno lile alilolisema Bwana juu ya Moabu zamani. 14 Lakini sasa Bwana asema hivi, Katika muda wa miaka mitatu, kama miaka ya mtu wa mshahara, utukufu wa Moabu utadharauliwa, pamoja na wingi wake wote; mabaki yake yatakuwa machache sana, kama si kitu kabisa.

Isaya 17

1 Ufunuo juu ya Dameski. Tazama, Dameski umeondolewa usiwe mji, nao utakuwa chungu ya magofu. 2 Miji ya Aroeri imeachwa; itakuwa kwa makundi ya kondoo, nao watajilaza huko wala hapana atakayewatia hofu. 3 Na ngome ya Efraimu itakomeshwa, na ufalme wa Dameski, na mabaki ya Shamu; watakuwa kama utukufu wa wana wa Israeli, asema Bwana wa majeshi. 4 Tena itakuwa katika siku hiyo, utukufu wa Yakobo utapungua-pungua, na kunona kwa mwili wake kutakonda. 5 Tena itakuwa kama hapo avunaye ashikapo mabua ya ngano, na mkono wake ukatapo masuke; tena itakuwa kama hapo mtu aokotapo masuke katika bonde la Warefai. 6 Lakini kilichosazwa na mvunaji kitakuwa ndani yake, kama vile wakati wa kupiga mizeituni, matunda mawili matatu yaliyo juu sana; matunda manne matano katika matawi, matawi ya mti wa matunda, asema Bwana, Mungu wa Israeli. 7 Katika siku hiyo mwanadamu atamwangalia Muumba wake, na macho yake yatamtazama Mtakatifu wa Israeli. 8 Wala hataziangalia madhabahu, kazi ya mikono yake; wala hatavitazama vilivyofanyika kwa vidole vyake, maashera na sanamu za jua. 9 Katika siku hiyo miji yake yenye maboma itakuwa kama mahali palipoachwa ndani ya mwitu, na juu ya kilele cha mlima, palipoachwa mbele ya wana wa Israeli; napo patakuwa ganjo. 10 Maana umemsahau Mungu wa wokovu wako, wala hukuukumbuka mwamba wa ngome yako; kwa sababu hiyo ulipanda mashamba yapendezayo, na kutia ndani yake mizabibu migeni. 11 Katika siku ile ulipopanda, ulifanya kitalu, na wakati wa asubuhi ulizimeesha mbegu zako, lakini mavuno yatatoweka siku ya huzuni, na ya sikitiko la moyo lifishalo. 12 Aha! Uvumi wa watu wengi! Wanavuma kama uvumi wa bahari; Aha! Ngurumo ya mataifa! Wananguruma kama ngurumo ya maji mengi; 13 Mataifa wananguruma kama ngurumo ya maji mengi; Lakini atawakemea, nao watakimbia mbali sana, Watafukuzwa kama makapi milimani mbele ya upepo, Na kama mavumbi vuruvuru mbele ya tufani. 14 Wakati wa jioni, tazama, kuna hofu; Na kabla ya mapambazuko hawako; Hilo ndilo fungu lao watutekao, Na ajali yao wanaotunyang'anya mali zetu.

Isaya 18

1 Ole wa nchi ya uvumi wa mabawa, Iliyoko mbali kupita mito ya Kushi; 2 Ipelekayo wajumbe wake kwa njia ya bahari, Na katika vyombo vya manyasi juu ya maji. Nendeni, wajumbe wepesi,kwa watu warefu,laini; Watu watishao tangu mwanzo wao hata sasa; Taifa la wenye nguvu,wakanyagao watu, Ambao mito inakata nchi yao. 3 Enyi watu mkaao katika ulimwengu wote, na wenyeji wa dunia, bendera ikiinuliwa milimani, angalieni; na wakipiga tarumbeta, sikieni. 4 Maana Bwana ameniambia hivi, Mimi nitatulia, na kuangalia katika makazi yangu, kama wakati wa mwangaza mweupe wa jua kali, mfano wa wingu la umande katika hari ya mavuno. 5 Maana kabla ya mavuno, maua yaangukapo, na maua yakawa zabibu zianzazo kuiva, ndipo atakapoyakata matawi kwa miundu, na kuviondoa vitawi vilivyopanuka na kuvikata. 6 Wote pamoja wataachiwa ndege wakali wa milimani, na hayawani wa nchi; ndege wakali watakaa juu yao wakati wa jua, na hayawani wote wa nchi watakaa juu yao wakati wa baridi. 7 Wakati huo Bwana wa majeshi ataletewa hedaya na watu warefu, laini; Watu watishao tangu mwanzo wao hata sasa; Taifa la wenye nguvu, wakanyagao watu, Ambao mito inakata nchi yao; mpaka mahali pa jina la Bwana wa majeshi,mlima Sayuni.

Isaya 19

1 Ufunuo juu ya Misri. Tazama, Bwana amepanda juu ya wingu jepesi, anafika Misri; na sanamu za Misri zinatikisika mbele zake, na moyo wa Misri unayeyuka ndani yake. 2 Nami nitawaamsha Wamisri juu ya Wamisri; nao watapigana, kila mtu na ndugu yake, na kila mtu na jirani yake, mji juu ya mji, na ufalme juu ya ufalme. 3 Na roho ya Misri itamwagika kabisa katikati yake, nami nitayabatilisha mashauri yake, nao watakwenda kwa sanamu zao, na kwa waganga, na kwa wapiga ramli, na kwa wachawi. 4 Nami nitawatoa hao Wamisri na kuwatia katika mikono ya bwana mgumu; na mfalme mkali atawatawala; asema Bwana, Bwana wa majeshi. 5 Na maji ya baharini yatapunguka, na huo mto utakauka na kuwa pakavu. 6 Na vijito vya mto vitatoa uvundo, na mifereji ya Misri itakuwa haina maji mengi, itakauka; manyasi na mianzi itanyauka. 7 Vitu vimeavyo karibu na Nile, katika ukingo wa Nile, na vyote vilivyopandwa karibu na Nile vitakauka na kuondolewa na kutoweka. 8 Na wavuvi wataugua, na wote wavuao kwa ndoana watahuzunika, nao watandao jarife juu ya maji watazimia. 9 Tena wao wafanyao kazi ya kuchana kitani watafadhaika, na hao pia wafumao bafta. 10 Na nguzo za nchi zitavunjika vipande vipande, wote wafanyao kazi ya mshahara watahuzunika nafsini mwao. 11 Wakuu wa Soani wamekuwa wapumbavu kabisa; washauri wenye hekima wa Farao, shauri lao limepumbazika; mwawezaje kumwambia Farao, Mimi ni mwana wa wenye hekima, ni mwana wa wafalme wa zamani? 12 Wako wapi, basi, watu wako wenye hekima? Na wakuambie sasa; na wajue mambo aliyokusudia Bwana wa majeshi juu ya Misri. 13 Wakuu wa Soani wamekuwa wapumbavu, wakuu wa Nofu wamedanganyika; na hao walio mawe ya pembeni ya kabila zake wameikosesha Misri. 14 Yeye Bwana ametia roho ya ushupavu katika moyo wa Misri, nao wameikosesha Misri katika matendo yake yote, kama mlevi aendavyo huko na huko akitapika. 15 Wala haitakuwako kazi yo yote katika Misri iwezayo kufanywa, ya kichwa au ya mkia, ya tawi au ya nyasi. 16 Katika siku hiyo Misri itakuwa kama wanawake; itatetemeka na kuogopa kwa sababu ya kutikiswa kwa mkono wa Bwana wa majeshi, autikisao juu yake. 17 Na nchi ya Yuda itakuwa sababu ya utisho kwa Misri; kila mtu atakayeambiwa habari zake ataingiwa na woga, kwa sababu ya kusudi la Bwana wa majeshi, analolikusudia juu yake. 18 Katika siku hiyo itakuwako miji mitano katika nchi ya Misri itumiayo lugha ya Kanaani, na kumwapia Bwana wa majeshi; mji mmoja utaitwa Mji wa uharibifu. 19 Katika siku hiyo itakuwako madhabahu katika nchi ya Misri kwa Bwana, na nguzo mpakani mwake kwa Bwana. 20 Nayo itakuwa ishara na ushuhuda kwa Bwana wa majeshi katika nchi ya Misri; kwa maana watamlilia Bwana kwa sababu ya watu wawaoneao, naye atawapelekea mwokozi mwenye kuwatetea, naye atawaokoa. 21 Na Bwana atajulikana na Misri, na Wamisri watamjua Bwana katika siku hiyo; naam watamtumikia kwa dhabihu na matoleo, nao watamwekea Bwana nadhiri, na kuzitekeleza. 22 Naye Bwana atapiga Misri, akipiga na kuponya; nao wakirudi kwa Bwana, atakubali maombi yao na kuwaponya. 23 Katika siku hiyo itakuwako njia kuu itokayo Misri na kufika hata Ashuru; Mwashuri atafika Misri, na Mmisri atafika Ashuru, na Wamisri wataabudu pamoja na Waashuri. 24 Katika siku hiyo Israeli atakuwa wa tatu pamoja na Misri na Ashuru, watakuwa baraka kati ya dunia; 25 kwa kuwa Bwana wa majeshi amewabariki, akisema, Wabarikiwe watu wangu Misri; na wewe Ashuru, kazi ya mikono yangu; na wewe Israeli, urithi wangu.

Isaya 20

1 Katika mwaka ule jemadari Yule alipofika Ashdodi,alipotumwa na Sargoni mfalme wa Ashuru;naye alipigana na Ashdodi akautwaa. 2 wakati huo Bwana alinena kwa kinywa cha Isaya, mwana wa Amozi, akisema, Haya, uvue nguo ya magunia viunoni mwako, na viatu vyako miguuni mwako. 3 Naye akafanya hivyo akaenda uchi, miguu yake haina viatu. Bwana akasema, Kama vile mtumishi wangu Isaya anavyokwenda uchi, hana viatu, awe ishara na ajabu kwa muda wa miaka mitatu juu ya Misri na juu ya Kushi; 4 vivyo hivyo mfalme wa Ashuru atawachukua uchi, wafungwa wa Misri, na watu wa Kushi waliohamishwa, watoto kwa wazee, hawana viatu, matako yao wazi, Misri iaibishwe. 5 Nao watafadhaika, na kuona haya kwa ajili ya Kushi, matumaini yao, na Misri, utukufu wao. 6 Na mwenyeji wa nchi ya pwani atasema katika siku hiyo, Angalia, haya ndiyo yaliyowapata watu wale tuliowatumaini, ambao tuliwakimbilia watuokoe na mfalme wa Ashuru; na sisi je! Twawezaje kupona?

Isaya 21

1 Ufunuo juu ya bara ya bahari. Kama tufani za Negebu zikaribiavyo kwa kasi,inakuja kutoka bara,toka nchi itishayo. 2 Nimeonyeshwa maono magumu; atendaye hila anatenda hila, mharibu anaharibu. Panda juu, Ee Elamu; husuru, Ee Umedi; mimi ninakomesha maombolezo yake yote. 3 Kwa sababu hiyo viuno vyangu vimejaa maumivu, utungu umenishika, kama utungu wa mwanamke azaaye; ninaumwa sana, nisiweze kusikia; nimefadhaishwa wa hofu, nisiweze kuona. 4 Moyo wangu unapiga-piga, utisho umenitaabisha, gizagiza la jioni nilipendalo limegeuka likanitetemesha. 5 Wanaandika meza, wanaweka ulinzi, wanakula, wanakunywa. Simameni, enyi wakuu, itieni ngao mafuta. 6 Maana Bwana ameniambia hivi, Enenda, weka mlinzi; aonayo na ayatangaze. 7 Naye akiona kundi la wapanda farasi, wakienda wawili wawili, na kundi la punda, na kundi la ngamia; asikilize sana, akijitahidi kusikiliza. 8 Ndipo akalia kama simba, Ee Bwana, mimi nasimama daima juu ya mnara wakati wa mchana, na kila usiku ninakaa katika zamu ya ulinzi wangu. 9 Na, tazama, linakuja kundi la watu, wapanda farasi, wakienda wawili wawili. Akajibu na kusema, Babeli umeanguka, umeanguka; na sanamu zote za miungu yake zimevunjwa chini. 10 Ewe niliyekufikicha, na nafaka ya sakafu yangu; Hayo niliyoyasikia kwa Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, nimewapasha habari zake. 11 Ufunuo juu ya Duma. Mtu ananililia toka Seiri, Ee mlinzi, habari gani za usiku? Ee mlinzi, habari gani za usiku? 12 Mlinzi akasema, Mchana unakuja na usiku pia; mkitaka kuuliza, ulizeni; njoni tena. 13 Ufunuo juu ya Arabuni. Ndani ya msitu wa Arabuni mtalala, Enyi misafara ya Wadedani. 14 Waleteeni wenye kiu maji, Enyi wenyeji wa nchi ya Tema; Nendeni kuwalaki wakimbiao na chakula chao. 15 Kwa maana wanakimbia mbele ya panga, Upanga uliofutwa, na upinde uliopindwa, Na mbele ya ukali wa vita. 16 Kwa sababu Bwana ameniambia hivi, Katika muda wa mwaka, kama miaka ya mtu mwenye kuajiriwa, utaangamia utukufu wote wa Kedari. 17 Na mabaki ya hesabu ya wavuta pinde, hao mashujaa wa Kedari watakuwa wachache; maana Bwana, Mungu wa Israeli, amenena neno hili.

Isaya 22

1 Ufunuo juu ya bonde la maono. Sasa una nini, wewe, Hata umepanda pia juu ya dari za nyumba? 2 Ewe uliyejaa makelele, Mji wa ghasia, mji wenye furaha; Watu wako waliouawa hawakuuawa kwa upanga, Wala hawakufa vitani. 3 Wakuu wako wote wamekimbia pamoja, Wamefungwa wasiutumie upinde. Wote walioonekana wamefungwa pamoja, Wamekimbia mbali sana. 4 Kwa sababu hiyo nasema, Geuza uso wako usinitazame, nipate kulia kwa uchungu; usijishughulishe kunifariji, kwa ajili ya kuharibika kwake binti ya watu wangu. 5 Kwa maana siku ya kutaabika, siku ya kukanyagwa, siku ya fujo inakuja, itokayo kwa Bwana, Bwana wa majeshi, katika bonde la Maono; inabomoa kuta; na kuililia milima. 6 Na Elamu wameshika podo, pamoja na magari ya vita, na watu wenye kupanda farasi; na Kiri wameifunua ngao. 7 Hata ikawa mabonde yako mateule yamejaa magari ya vita, nao wapandao farasi wamejipanga wakielekea malango. 8 Kisha alikiondoa kifuniko cha Yuda, nawe siku hiyo ulivitazama vyombo vya vita katika nyumba ya mwituni. 9 Nanyi mlipaona mahali palipobomoka katika mji wa Daudi ya kuwa ni pengi, nanyi mliyakusanya maji ya birika la chini. 10 Nanyi mlizihesabu nyumba za Yerusalemu, mkazibomoa nyumba ili kuutia nguvu ukuta. 11 Nanyi mlifanya birika la maji katikati ya kuta mbili, la kuwekea maji ya birika la kale; lakini hamkumwangalia yeye aliyeyafanya hayo, wala kumjali yeye aliyeyatengeneza zamani. 12 Siku hiyo Bwana, Bwana wa majeshi, akawaita watu walie na kuomboleza, na kung'oa nywele zao, na kuvaa nguo za magunia; 13 na kumbe! Furaha, na kuchekelea, na kuchinja ng'ombe, na kuchinja kondoo, na kula nyama, na kunywa mvinyo; tule, tunywe, kwa maana kesho tutakufa. 14 Na yeye Bwana wa majeshi akafunua haya masikioni mwangu, Ni kweli, uovu huu hautatakaswa wala kuwatokeni hata mfe; asema Bwana, Bwana wa majeshi. 15 Bwana, Bwana wa majeshi, asema hivi, Haya! Enenda kwa huyu mtunza hazina, yaani, Shebna, aliye juu ya nyumba, ukamwambie, 16 Unafanyaje hapa? Nawe una nani hapa? Hata ukachimba kaburi hapa; ukamchimbia kaburi huko juu, na kumchongea makao katika jabali! 17 Tazama, Bwana atakutupa kwa nguvu, kama mtu mwenye nguvu; naam, atakuzonga-zonga. 18 Hakika atakukunja na kukutupa kama mpira, mpaka nchi iliyo mbali; huko utakufa, na magari ya utukufu wako yatakuwa kuko huko, ewe uliye aibu ya nyumba ya bwana wako. 19 Nami nitakusukuma na kukutoa katika mahali pako, naye atakushusha utoke hapa usimamapo. 20 Na itakuwa katika siku ile nitamwita mtumishi wangu Eliakimu, mwana wa Hilkia; 21 nami nitamvika vazi lako, nitamtia nguvu kwa mshipi wako, nami nitamkabidhi yeye mamlaka yako; naye atakuwa baba kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa nyumba ya Yuda. 22 Na ufunguo wa nyumba ya Daudi nitauweka begani mwake; yeye atafungua wala hapana atakayefunga; naye atafunga wala hapana atakayefungua. 23 Nami nitamkaza kama msumari mahali palipo imara; naye atakuwa kiti cha utukufu kwa nyumba ya baba yake. 24 Nao wataangika juu yake utukufu wote wa nyumba ya baba yake; wazao wake na watoto wao, kila chombo kidogo tangu vyombo vya vikombe hata vyombo vya makopo vyote pia. 25 Katika siku ile, asema Bwana wa majeshi, ule msumari uliokazwa katika mahali palipo imara utalegea; nao utakatwa na kuanguka chini, na ule mzigo uliokuwa juu yake utakatiliwa mbali; maana Bwana amesema haya.

Isaya 23

1 Ufunuo juu ya Tiro. Toeni sauti za uchungu, enyi merikebu za Tarshishi, kwa maana umeharibika kabisa, hata hapana nyumba, hapana mahali pa kuingia; toka nchi ya Kitimu wamefunuliwa habari. 2 Tulieni, enyi mkaao kisiwani; wewe ambaye wafanya biashara wa Sidoni, wavukao bahari, walikujaza. 3 Vitu vilivyopandwa, vya Shihori, mavuno ya Nile, yaliyokuja juu ya maji mengi, ndiyo pato lake, naye alikuwa soko la mataifa. 4 Tahayari, Ee Sidoni; kwa maana bahari imenena, hiyo ngome ya bahari ilisema, Sikuona utungu, wala sikuzaa, wala sikulea vijana, wala sikulea wanawali. 5 Habari itakapofika Misri wataona uchungu sana kwa sababu ya habari ya Tiro. 6 Piteni mpaka Tarshishi, enyi mkaao kisiwani, toeni sauti ya uchungu. 7 Je! Huu ndio mji wenu wa furaha, ambao mwanzo wake ulikuwako tangu siku za kale, ambao miguu yake ilimchukua akae mbali sana? 8 Ni nani aliyefanya shauri hili juu ya Tiro, uliotia watu taji, ambao wafanya biashara wake walikuwa wana wa wafalme, na wachuuzi wake ni watu wakuu wa dunia? 9 Bwana wa majeshi ndiye aliyefanya shauri hili, ili kuharibu kiburi cha utukufu wote, na kuwaaibisha watu wa duniani wote pia. 10 Pita katika nchi yako, kama Nile, Ee binti wa Tarshishi, hapana tena mshipi wa kukuzuia. 11 Amenyosha mkono wake juu ya bahari, amezitikisa falme; Bwana ametoa amri katika habari za Kanaani, kuziangamiza ngome zake. 12 Naye akasema, Usizidi kufurahi, ewe bikira uliyeaibishwa, binti wa Sidoni, haya, ondoka, uende hata Kitimu; huko nako hutapata raha. 13 Tazama, nchi ya Wakaldayo; watu hao hawako tena; Mwashuri ameiweka tayari kwa hayawani wa jangwani; wamesimamisha buruji zao za vita, wameyaharibu majumba yake ya enzi, akaufanya kuwa uharibifu. 14 Pigeni yowe, enyi merikebu za Tarshishi; maana ngome yenu imefanywa ukiwa. 15 Basi, itakuwa katika siku ile, Tiro utasahauliwa miaka sabini, kadiri ya siku za mfalme mmoja; hata mwisho wa miaka sabini, Tiro utakuwa kama vile ulivyo wimbo wa kahaba. 16 Twaa kinubi, tembea mjini, Ewe kahaba uliyesahauliwa; Piga vizuri, imba nyimbo nyingi, Upate kukumbukwa tena. 17 Hata itakuwa mwisho wa miaka sabini, Bwana ataizuru nchi ya Tiro, naye atarudi apate ujira wake, atafanya ukahaba pamoja na falme zote za ulimwengu juu ya uso wa dunia. 18 Na biashara yake na ujira wake utakuwa wakfu kwa Bwana, hautawekwa hazinani wala hautawekwa akiba; bali mapato ya biashara yake yatakuwa mali zao wakaao mbele za Bwana, wapate kula na kushiba, na kuvaa mavazi ya fahari.

Isaya 24

1 Tazama, Bwana ameifanya dunia kuwa tupu, aifanya ukiwa, aipindua, na kuwatawanya wakaao ndani yake. 2 Na itakuwa kama ilivyo hali ya watu, ndivyo itakavyokuwa hali ya kuhani; kama ilivyo hali ya mtumwa, ndivyo itakavyokuwa hali ya bwana wake; kama ilivyo hali ya mjakazi, ndivyo itakavyokuwa hali ya bibi yake; kama ilivyo hali yake anunuaye, ndivyo itakavyokuwa hali yake auzaye; kama ilivyo hali yake akopeshaye, ndivyo itakavyokuwa hali yake akopaye; kama ilivyo hali yake atwaaye faida, ndivyo itakavyokuwa hali yake ampaye faida. 3 Dunia hii itafanywa tupu kabisa, na kuharibiwa kabisa; maana Bwana amenena neno hilo. 4 Dunia inaomboleza, inazimia; ulimwengu unadhoofika, unazimia; watu wakuu wa dunia wanadhoofika. 5 Tena dunia imetiwa unajisi kwa watu wanaoikaa; kwa maana wameziasi sheria, wameibadili amri, wamelivunja agano la milele. 6 Ndiyo sababu laana imeila dunia hii, na hao wanaoikaa wameonekana kuwa na hatia, ndiyo sababu watu wanaoikaa dunia wameteketea, watu waliosalia wakawa wachache tu. 7 Divai mpya inaomboleza, mzabibu umedhoofika, watu wote waliochangamka moyo wanaugua. 8 Sauti ya furaha ya matoazi inakoma; kelele yao wafurahio imekwisha; furaha ya kinubi inakoma. 9 Hawatakunywa divai pamoja na nyimbo; kileo kitakuwa uchungu kwao wakinywao. 10 Mji wa machafuko umebomolewa; kila nyumba imefungwa, asipate kuingia mtu awaye yote. 11 Pana kilio katika njia kuu kwa sababu ya divai; furaha yote imetiwa giza, na changamko la nchi limetoweka. 12 Ndani ya mji umebaki ukiwa, na lango lake limepigwa kwa uharibifu. 13 Maana katikati ya dunia, katikati ya mataifa, itakuwa hivi; kama wakati utikiswapo mzeituni, kama wakati waokotapo zabibu baada ya mavuno yake. 14 Hawa watainua sauti zao, watapiga kelele; kwa sababu ya utukufu wa Bwana watapiga kelele toka baharini. 15 Basi, mtukuzeni Bwana katika mashariki, litukuzeni jina la Bwana, Mungu wa Israeli, katika visiwa vya bahari. 16 Toka pande za mwisho wa dunia tumesikia nyimbo, Atukuzwe mwenye haki. Ndipo niliposema, Kukonda kwangu! Kukonda kwangu! Ole wangu! Watenda hila wametenda hila, naam, watendao hila wametenda hila sana. 17 Hofu, na shimo, na mtego, vi juu yako, Ee mwenye kukaa duniani. 18 Itakuwa kila akimbiaye sauti ya hofu ataanguka katika shimo; na kila apandaye na kutoka shimoni atanaswa na mtego; kwa maana madirisha yaliyo juu yamewekwa wazi, na misingi ya dunia inatikisika. 19 Dunia kuvunjika, inavunjika sana; dunia kupasuka, imepasuka sana; dunia kutikisika, imetikisika sana. 20 Dunia inalewa-lewa kama mlevi, nayo inawaya-waya kama machela; na mzigo wa dhambi zake utailemea; nayo itaanguka, wala haitainuka tena. 21 Tena itakuwa katika siku hiyo, Bwana ataliadhibu jeshi la mahali palipo juu katika mahali palipo juu, na wafalme wa dunia katika dunia; 22 nao watakusanywa pamoja kama vile wakusanywavyo wafungwa katika shimo nao watafungwa katika gereza; na baada ya muda wa siku nyingi watajiliwa. 23 Ndipo mwezi utatahayari, na jua litaona haya; kwa kuwa Bwana wa majeshi atatawala katika mlima wa Sayuni, na katika Yerusalemu, na mbele ya wazee wake kwa utukufu.

Isaya 25

1 Ee Bwana, wewe u Mungu wangu; Nitakutukuza na kulihimidi jina lako; Kwa kuwa umetenda mambo ya ajabu, Mashauri ya kale, kwa uaminifu na kweli. 2 Kwa sababu umefanya mji kuwa ni chungu; Mji wenye boma kuwa ni magofu; Jumba la wageni kuwa si mji; Hautajengwa tena milele. 3 Kwa hiyo watu walio hodari watakutukuza, Mji wa mataifa watishao utakuogopa. 4 Maana umekuwa ngome ya maskini, Ngome ya mhitaji katika dhiki yake, Mahali pa kukimbilia wakati wa tufani, Kivuli wakati wa hari; Wakati uvumapo upepo wa watu watishao, Kama dhoruba ipigayo ukuta. 5 Kama vile hari katika mahali pakavu Utaushusha mshindo wa wageni; Kama ilivyo hari kwa kivuli cha wingu, Wimbo wa hao watishao utashushwa. 6 Na katika mlima huu Bwana wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana. 7 Naye katika mlima huu atauharibu uso wa sitara iliyowekwa juu ya watu wote, na utaji ule uliotandwa juu ya mataifa yote. 8 Amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU atafuta machozi katika nyuso zote; na aibu ya watu wake ataiondoa katika ulimwengu wote; maana Bwana amenena hayo. 9 Katika siku hiyo watasema, Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, Ndiye tuliyemngoja atusaidie; Huyu ndiye Bwana tuliyemngoja, Na tushangilie na kuufurahia wokovu wake. 10 Kwa maana mkono wa Bwana utatulia katika mlima huu, na Moabu atakanyagwa chini huko aliko, kama vile majani makavu yakanyagwavyo katika maji ya jaa. 11 Naye atanyosha mikono yake katikati yake, kama vile aogeleaye anyoshavyo mikono yake ili aogelee, naye atashusha kiburi chake, pamoja na hila za mikono yake. 12 Na boma la ngome ya kuta zako ameliinamisha, na kulilaza chini, na kulitupa chini hata mavumbini.

Isaya 26

1 Siku ile wimbo huu utaimbwa katika nchi ya Yuda; Sisi tunao mji ulio na nguvu; Ataamuru wokovu kuwa kuta na maboma. 2 Wekeni wazi malango yake, Taifa lenye haki, lishikalo kweli, liingie. 3 Utamlinda yeye ambaye moyo wake umekutegemea Katika amani kamilifu, kwa kuwa anakutumaini. 4 Mtumainini Bwana siku zote Maana Bwana YEHOVA ni mwamba wa milele. 5 Kwa kuwa amewashusha wakaao juu, Mji ule ulioinuka, aushusha, Aushusha hata nchi, auleta hata mavumbini. 6 Mguu utaukanyaga chini, Naam, miguu yao walio maskini, Na hatua zao walio wahitaji. 7 Njia yake mwenye haki ni unyofu; Wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki. 8 Naam, katika njia ya hukumu zako Sisi tumekungoja, Ee Bwana; Shauku ya nafsi zetu inaelekea Jina lako na ukumbusho wako. 9 Kwa nafsi yangu nimekutamani wakati wa usiku; Naam, kwa nafsi yangu ndani yangu nitakutafuta mapema; Maana hukumu zako zikiwapo duniani, Watu wakaao duniani hujifunza haki. 10 Mtu mbaya ajapofadhiliwa, Hata hivyo hatajifunza haki; Katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu, Wala hatauona utukufu wa Bwana. 11 Bwana, mkono wako umeinuliwa, lakini hawaoni; lakini watauona wivu wako kwa ajili ya watu wako, nao watatahayari; naam, moto utawala adui zako. 12 Bwana, utatuamuria amani; maana ni wewe pia uliyetutendea kazi zetu zote. 13 Ee Bwana, Mungu wetu, mabwana wengine zaidi ya wewe wametumiliki; lakini kwa msaada wako peke yako tutalitaja jina lako. 14 Wao wamekufa, hawataishi; wamekwisha kufariki, hawatafufuka; kwa sababu hiyo umewajilia, na kuwaangamiza, na kuupoteza ukumbusho wao. 15 Umeliongeza hilo taifa, Bwana, umeliongeza taifa; wewe umetukuzwa, umeipanua mipaka yote ya nchi hii. 16 Bwana, katika taabu zao walikwenda kwako; waliomba maombi mengi wakati adhabu yako ilipokuwa juu yao. 17 Kama vile mwanamke mwenye mimba anayekaribia wakati wake wa kuzaa, alivyo na utungu na kulia kwa sababu ya maumivu yake, ndivyo tulivyokuwa sisi mbele zako, Ee Bwana. 18 Tumekuwa na mimba, tumekuwa na utungu, tumekuwa kana kwamba tumezaa upepo; hatukufanya wokovu wo wote duniani, wala hawakuanguka wakaao duniani. 19 Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea, nayo ardhi itawatoa waliokufa. 20 Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. 21 Kwa maana, tazama, Bwana anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.

Isaya 27

1 Katika siku hiyo Bwana, kwa upanga wake ulio mkali, ulio mkubwa, ulio na nguvu, atamwadhibu lewiathani, nyoka yule mwepesi, na lewiathani, nyoka yule mwenye kuzonga-zonga; naye atamwua yule joka aliye baharini. 2 Katika siku hiyo; Shamba la mizabibu la mvinyo, liimbieni. 3 Mimi, Bwana, nalilinda, Nitalitia maji kila dakika, Asije mtu akaliharibu; Usiku na mchana nitalilinda. 4 Hasira sinayo ndani yangu; Kama mibigili na miiba ingekuwa mbele zangu, Ningepanga vita juu yake, Ningeiteketeza yote pamoja. 5 Au azishike nguvu zangu, Afanye amani nami; Naam, afanye amani nami. 6 Siku zijazo Yakobo atatia mizizi; Israeli atatoa maua na kuchipuka; Nao watajaza uso wa ulimwengu matunda. 7 Je! Amempiga kama hilo pigo la hao waliompiga, au ameuawa kama walivyouawa wao waliouawa na yeye? 8 Umemwadhibu kwa kiasi, ulipomfukuza; ukampepeta kwa upepo mkali katika siku ya upepo wa mashariki. 9 Basi, uovu wa Yakobo utatakaswa hivyo, na hayo ndiyo matunda yote ya kumwondolea dhambi yake; afanyapo mawe yote ya madhabahu kuwa kama mawe ya chokaa yaliyopondwa, hata maashera na sanamu za jua havitasimama tena. 10 Kwa maana mji ulio na boma umekuwa peke yake, makao yaliyoachwa na ukiwa kama jangwa; huko ndiko atakakolisha ndama, na huko ndiko atakakolala, na kuyala matawi yake. 11 Matawi yake yatakapokauka yatavunjwa; wanawake watakuja na kuyachoma moto; kwa maana hawa si watu wenye akili; kwa sababu hiyo yeye aliyewaumba hatawahurumia, yeye aliyewafanya hatawasamehe. 12 Tena itakuwa katika siku hiyo, Bwana atayapiga-piga matunda yake toka gharika ya Mto hata kijito cha Misri, nanyi mtakusanywa mmoja mmoja, enyi wana wa Israeli. 13 Tena itakuwa katika siku hiyo, tarumbeta kubwa itapigwa, nao waliokuwa karibu na kuangamia katika nchi ya Ashuru watakuja; na hao waliotupwa katika nchi ya Misri; nao watamsujudu Bwana katika mlima mtakatifu huko Yerusalemu.

Isaya 28

1 Ole wa taji ya kiburi ya walevi wa Efraimu, na ua la uzuri wa fahari yake linalonyauka, lililo kichwani mwa bonde linalositawi, la hao walioshindwa na divai! 2 Tazama, Bwana ana mmoja aliye hodari, mwenye nguvu; kama dhoruba ya mvua ya mawe, tufani iharibuyo, kama dhoruba ya maji mengi yafurikayo, ndivyo atakavyotupa chini kwa mkono. 3 Taji ya kiburi ya walevi wa Efraimu itakanyagwa kwa miguu; 4 na ua la uzuri wa fahari yake linalonyauka, lililo kichwani mwa bonde linalositawi, litakuwa kama tini iliyotangulia kuiva kabla ya wakati wa hari, ambayo, aionapo yeye aiangaliaye, huila mara anapoishika mkononi mwake. 5 Katika siku ile Bwana wa majeshi atakuwa ni taji ya fahari, na kilemba cha uzuri, kwa mabaki ya watu wake. 6 Naye atakuwa roho ya hukumu kwake yeye aketiye ili ahukumu; naye atakuwa nguvu kwao wageuzao nyuma vita langoni. 7 Lakini hawa nao wamekosa kwa divai, wamepotea kwa kileo; kuhani na nabii wamekosa kwa kileo, wamemezwa kwa divai, wamepotea kwa kileo; hukosa katika maono, hujikwaa katika hukumu. 8 Maana meza zote zimejaa matapiko na uchafu, hapana mahali palipo safi. 9 Atamfundisha nani maarifa? Atamfahamisha nani habari hii? Je! Ni wale walioachishwa maziwa, walioondolewa matitini? 10 Kwa maana ni amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo. 11 La, bali kwa midomo ya watu wageni, na kwa lugha nyingine atasema na watu hawa; 12 ambao aliwaambia, Hii ndiyo raha yenu, mpeni raha yeye aliyechoka; huku ndiko kuburudika; lakini hawakutaka kusikia. 13 Kwa sababu hiyo neno la Bwana kwao litakuwa hivi, amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo; ili waende na kuanguka nyuma, na kuvunjwa, na kunaswa, na kuchukuliwa. 14 Basi, lisikieni neno la Bwana, enyi watu wenye dharau, mnaowatawala watu hawa walio ndani ya Yerusalemu. 15 Kwa sababu mmesema, Tumefanya agano na mauti, tumepatana na kuzimu; pigo lifurikalo litakapopita, halitatufikia sisi; kwa maana tumefanya maneno ya uongo kuwa kimbilio letu, tumejificha chini ya maneno yasiyo kweli; 16 kwa ajili ya hayo Bwana, MUNGU, asema hivi, Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara; yeye aaminiye hatafanya haraka. 17 Nami nitafanya hukumu kuwa ndiyo kanuni, na haki kuwa ndiyo timazi; na mvua ya mawe itachukulia mbali hilo kimbilio la maneno ya uongo, na maji yatapagharikisha mahali pa kujisitiri. 18 Na agano lenu mliloagana na mauti litabatilika, tena mapatano yenu mliyopatana na kuzimu hayatasimama; pigo lifurikalo litakapopita, ndipo ninyi mtakapokanyagwa nalo. 19 Kila wakati litakapopita litawachukueni. Maana litapita asubuhi baada ya asubuhi, wakati wa mchana na wakati wa usiku; na kuifahamu habari ile kutakuwa kitisho tu. 20 Maana kitanda kile ni kifupi asiweze mtu kujinyosha juu yake, na nguo ile ya kujifunika ni nyembamba asipate mtu kujizingisha. 21 Maana Bwana ataondoka kama vile katika mlima Perasimu, ataghadhibika kama vile katika bonde la Gibeoni; apate kufanya kazi yake, kazi yake ya ajabu; na kulitimiza tendo lake, tendo lake la ajabu. 22 Basi sasa msiwe watu wenye kudharau, vifungo vyenu msije vikakazwa; maana nimesikia kwa Bwana, Bwana wa majeshi, habari ya hukumu itakayotimizwa, nayo imekusudiwa, itakayoipata dunia yote pia. 23 Tegeni masikio, sikieni sauti yangu, sikilizeni mkasikie neno langu. 24 Je! Mwenye kulima alima daima, ili apande? Afunua daima madongoa ya nchi yake, na kuyavunja? 25 Akiisha kuulainisha uso wa nchi yake, je! Hamwagi huko na huko kunde, na kutupa-tupa jira, na kuitia ngano safu safu, na shayiri mahali pake palipochaguliwa, na kusemethi karibu na mipaka yake? 26 Kwa maana Mungu wake anamwagiza vizuri na kumfundisha. 27 Kwa maana kunde zile hazipurwi kwa chombo kikali, wala gurudumu la gari halipitishwi huko na huko juu ya jira ile, bali kunde zile hupurwa kwa fimbo, na jira ile kwa ufito. 28 Ngano ya mkate husagwa; kwa maana haipuri siku zote bila kukoma; na ingawa gurudumu la gari lake na farasi wake huitawanya ngano ile, haisagi. 29 Hayo nayo yatoka kwa Bwana wa majeshi, mwenye shauri la ajabu, apitaye wote kwa hekima yake.

Isaya 29

1 Ole wa Arieli, Arieli, mji ambao Daudi alifanya kituo chake ndani yake; ongezeni mwaka baada ya mwaka; sikukuu na zirudi wakati wake, 2 ndipo nitamwudhi Arieli; kutakuwapo maombolezo na kilio; naye atakuwa kwangu kama Arieli. 3 Nami nitapiga kimo juu yako pande zote, nitakuhusuru kwa ngome, nami nitajenga maboma yakuzunguke. 4 Nawe utashushwa, nawe utanena toka chini ya nchi, na maneno yako yatakuwa chini toka mavumbini; na sauti yako itakuwa kama sauti ya mtu mwenye pepo, ikitoka katika nchi, na matamko yako yatanong'ona toka mavumbini. 5 Lakini wingi wa adui zako utakuwa kama mavumbi membamba, na wingi wao watishao utakuwa kama makapi yapitayo; naam, itakuwa mara na kwa ghafula. 6 Naye atajiliwa na Bwana wa majeshi kwa ngurumo, na tetemeko la nchi, na sauti kuu, na chamchela, na tufani, na mwali wa moto uteketezao. 7 Na wingi wa mataifa wapiganao na Arieli, wote wapiganao naye na ngome yake, nao wamwudhio, watakuwa kama ndoto, na maono ya usiku. 8 Tena itakuwa kama mtu mwenye njaa aotapo, kumbe, anakula; lakini aamkapo, nafsi yake haina kitu; na kama mtu mwenye kiu aotapo, kumbe, anakunywa; lakini aamkapo, kumbe, anazimia, na nafsi yake inatamani; hivyo ndivyo utakavyokuwa huo wingi wa mataifa waletao vita juu ya mlima Sayuni. 9 Ngojeni mstaajabu; fanyeni anasa zenu na kuwa vipofu; wamelewa wala si kwa mvinyo; wamewaya-waya wala si kwa sababu ya kileo. 10 Kwa maana Bwana amewamwagieni roho ya usingizi, amefumba macho yenu, yaani, manabii; amefunika vichwa vyenu, yaani, waonaji. 11 Na maono yote yamekuwa kwenu kama maneno ya chuo kilichotiwa muhuri, ambacho watu humpa mtu aliye na maarifa, wakisema, Tafadhali ukisome hiki; akasema, Siwezi, kwa kuwa kimetiwa muhuri; 12 kisha chuo hiki apewa mtu asiye na maarifa, akaambiwa, Kisome hicho tafadhali, akasema, Sina maarifa mimi. 13 Bwana akanena, Kwa kuwa watu hawa hunikaribia na kuniheshimu kwa vinywa vyao, bali mioyo yao wamefarakana nami, na kicho chao walicho nacho kwangu ni maagizo ya wanadamu waliyofundishwa; 14 kwa sababu hiyo mimi nitafanya tena kazi ya ajabu kati ya watu hawa, kazi ya ajabu na mwujiza; na akili za watu wao wenye akili zitapotea, na ufahamu wa wenye busara wao utafichwa. 15 Ole wao wanaojitahidi kumficha Bwana mashauri yao, na matendo yao yamo gizani, nao husema, Ni nani atuonaye? Nani atujuaye? 16 Ninyi mnapindua mambo; Je! Mfinyanzi ahesabiwe kuwa kama udongo; kitu kilichofinyangwa kimnene yeye aliyekifinyanga, Hakunifinyanga huyu; au kitu kilichoumbwa kimnene yeye aliyekiumba, Yeye hana ufahamu? 17 Je! Si muda mdogo uliobaki, na Lebanoni itageuzwa kuwa shamba lizaalo sana, na lile shamba lizaalo sana litahesabiwa kuwa msitu? 18 Na katika siku hiyo viziwi watasikia maneno ya hicho chuo, na macho ya vipofu yataona katika upofu na katika giza. 19 Wanyenyekevu nao wataongeza furaha yao katika Bwana, na maskini katika wanadamu watafurahi katika Mtakatifu wa Israeli. 20 Kwa maana mwenye kutisha ameangamizwa, naye mwenye dharau amekoma, nao wote watazamiao uovu wamekatiliwa mbali; 21 hao wamfanyao mtu kuwa amekosa katika neno, na kumtegea mtego yeye aonyaye langoni, na kumgeuza mwenye haki kwa kitu kisichofaa. 22 Basi, Bwana aliyemkomboa Ibrahimu asema hivi, katika habari za nyumba ya Yakobo; Yakobo hatatahayarika sasa, wala uso wake hautabadilika rangi yake. 23 Bali atakapowaona watoto wake, walio kazi ya mikono yangu, katikati yake, wao watalitakasa jina langu; naam, watamtakasa Mtakatifu wa Yakobo, nao watamcha Mungu wa Israeli. 24 Hao nao wakosao rohoni mwao watapata kufahamu, na hao wanung'unikao watajifunza elimu.

Isaya 30

1 Ole wa watoto waasi; asema Bwana; watakao mashauri lakini hawayataki kwangu mimi; wajifunikao kifuniko lakini si cha roho yangu; wapate kuongeza dhambi juu ya dhambi; 2 waendao kutelemkia Misri wala hawakuuliza kinywani mwangu; ili wajitie nguvu kwa nguvu za Farao, na kutumainia kivuli cha Misri. 3 Basi, nguvu za Farao zitakuwa aibu yenu, na kutumainia kivuli cha Misri kutakuwa kufadhaika kwenu. 4 Kwa maana wakuu wake wako Soani, na wajumbe wake wamefika Hanesi. 5 Wote watawaonea haya watu wasioweza kuwafaidia, wasio na msaada wala faida, bali ni aibu na sababu ya kushutumiwa. 6 Ufunuo juu ya hayawani wa Negebu. Katikati ya nchi ya taabu na dhiki, Ambayo hutoka huko simba jike na simba, Nyoka na joka la moto arukaye, Huchukua mali zao mabegani mwa punda wachanga, Na hazina zao juu ya nundu za ngamia Waende kwa watu ambao hawatawafaa kitu. 7 Kwa maana Misri huwasaidia bure, bila faida; Kwa hiyo nimemwita, Rahabu aketiye kimya. 8 Haya, enenda sasa, andika neno hili katika kibao mbele ya macho yao, lichore katika kitabu ili liwe kwa ajili ya majira yatakayokuja, kwa ushuhuda hata milele. 9 Kwa maana watu hawa ni watu waasi, watoto wasemao uongo, watoto wasiotaka kuisikia sheria ya Bwana; 10 wawaambiao waonaji, Msione; na manabii, Msitoe unabii wa mambo ya haki, tuambieni maneno laini, hubirini maneno yadanganyayo; 11 tokeni katika njia, geukeni mtoke katika mapito; mkomesheni Mtakatifu wa Israeli mbele yetu. 12 Basi kwa ajili ya hayo Mtakatifu wa Israeli asema hivi, Kwa sababu mwalidharau neno hili, na kutumainia jeuri na ukaidi, na kuyategemea hayo; 13 basi, uovu huu utakuwa kwenu kama mahali palipobomoka, palipo tayari kuanguka patokezapo katika ukuta mrefu, ambapo kuvunjika kwake huja ghafula kwa mara moja. 14 Naye atapavunja kama chombo cha mfinyanzi kivunjwavyo, akikivunja-vunja asiache kukivunja, hata hakipatikani katika vipande vyake kigae kitoshacho kutwaa moto jikoni, au kuteka maji kisimani. 15 Kwa maana Bwana MUNGU, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi, Kwa kurudi na kustarehe mtaokolewa; nguvu zenu zitakuwa katika kutulia na kutumaini; lakini hamkukubali. 16 Bali ninyi mlisema, La! Maana tutakimbia juu ya farasi; basi, ni kweli, mtakimbia; tena, Sisi tutakimbia juu ya wanyama waendao upesi; basi, wale watakaowafuatia watakuwa wepesi. 17 Elfu moja watakimbia kwa kukemewa na mtu mmoja; kwa kukemewa na watano mtakimbia; hata mtakapoachwa kama mlingoti juu ya kilele cha mlima, na kama bendera juu ya kilima. 18 Kwa ajili ya hayo Bwana atangoja, ili awaonee huruma, na kwa ajili ya hayo atatukuzwa, ili awarehemu; kwa maana Bwana ni Mungu wa hukumu; heri wote wamngojao. 19 Kwa maana watu watakaa katika Sayuni huko Yerusalemu; wewe hutalia tena; hakika yake atakuonea rehema nyingi kwa sauti ya kilio chako; asikiapo ndipo atakapokujibu. 20 Na ingawa Bwana atawapeni chakula cha shida na maji ya msiba, lakini waalimu wako hawatafichwa tena, ila macho yako yatawaona waalimu wako; 21 na masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto. 22 Nanyi mtakitia najisi kifuniko cha sanamu zenu za fedha zilizochongwa, na mabamba ya sanamu zenu za dhahabu zilizoyeyushwa; utazitupilia mbali kama kitu kilicho najisi; utasema, Haya, toka hapa. 23 Naye atatoa mvua juu ya mbegu zako, upate kuipanda nchi hii; na mkate wa mazao ya nchi, nayo itasitawi na kuzaa tele; katika siku hiyo ng'ombe zako watakula katika malisho mapana. 24 Ng'ombe pia na wana-punda wailimao nchi watakula chakula kilichokolea, kilichopepetwa kwa ungo na kwa pepeo. 25 Na juu ya kila mlima mrefu, na juu ya kila kilima kilichoinuka, itakuwapo mito na vijito vya maji, katika siku ya machinjo makuu itakapoanguka minara. 26 Na tena nuru ya mwezi itakuwa kama nuru ya jua, na nuru ya jua itaongezeka mara saba, kama nuru ya siku saba, katika siku ile Bwana atakapofunga mapigo ya watu wake, na kuliponya pigo la jeraha yao. 27 Tazama, jina la Bwana linakuja kutoka mbali sana, linawaka kwa hasira yake, kwa moshi mwingi sana unaopaa juu; midomo yake imejaa ghadhabu, na ulimi wake ni moto ulao; 28 na pumzi yake ni kijito kifurikacho, kifikacho hata shingoni, kupepeta mataifa kwa ungo wa ubatili; na lijamu ikoseshayo itakuwa katika taya za watu. 29 Mtakuwa na wimbo kama vile wakati wa usiku, ishikwapo sikukuu takatifu, mtakuwa na furaha ya moyo kama vile mtu aendapo na filimbi katika mlima wa Bwana, aliye Mwamba wa Israeli. 30 Naye Bwana atawasikizisha watu sauti yake ya utukufu, naye atawaonyesha jinsi mkono wake ushukavyo, na ghadhabu ya hasira yake, na mwako wa moto ulao, pamoja na dhoruba, na tufani, na mvua ya mawe ya barafu. 31 Maana kwa sauti ya Bwana, Mwashuri atavunjika-vunjika, yeye apigaye kwa bakora. 32 Na kila pigo la fimbo iliyoamriwa, ambayo Bwana ataliweka juu yake, litakuwa pamoja na matari na vinanda, na kwa mapigano yenye kutikisa atapigana nao. 33 Maana Tofethi imewekwa tayari tokea zamani, naam, imewekwa tayari kwa mfalme huyo; ameifanya kubwa, inakwenda chini sana; tanuru yake ni moto na kuni nyingi; pumzi ya Bwana, kama mto wa kiberiti, huiwasha.

Isaya 31

1 Ole wao watelemkao kwenda Misri wapate msaada, na kutegemea farasi; watumainio magari kwa kuwa ni mengi, na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli, wala hawamtafuti Bwana! 2 Lakini yeye naye ana akili, naye ataleta uovu, wala hatayatangua maneno yake; bali ataondoka juu ya nyumba yao watendao mabaya, na juu ya msaada wa hao watendao maovu. 3 Basi Wamisri ni wanadamu wala si Mungu, na farasi zao ni nyama wala si roho; na Bwana atakaponyosha mkono wake, yeye asaidiaye atajikwaa, na yeye asaidiwaye ataanguka, nao wote pamoja watakoma. 4 Maana Bwana aniambia hivi, Kama vile ilivyo simba angurumapo na mwana-simba juu ya mawindo yake, wachungaji wengi wakiitwa ili kumpiga, lakini hatiwi hofu na sauti zao, wala kufanya woga kwa sababu ya mshindo wao; ndivyo Bwana wa majeshi atakavyoshuka ili kufanya vita juu ya mlima Sayuni, na juu ya kilima chake. 5 Kama ndege warukao, Bwana wa majeshi ataulinda Yerusalemu; ataulinda na kuuokoa, atapita juu yake na kuuhifadhi. 6 Mwelekeeni yeye mliyemwasi sana, enyi wana wa Israeli. 7 Maana katika siku hiyo kila mtu atatupa sanamu zake za fedha, na sanamu zake za dhahabu, ambazo mikono yenu imezifanya, zikawa dhambi kwenu. 8 Ndipo huyo Mwashuri ataanguka kwa upanga ambao si wa mtu; na upanga usio upanga wa mtu utamla; naye ataukimbia upanga, na vijana wake watatoa kodi. 9 Na mwamba wake utatoweka kwa sababu ya hofu, nao wakuu wake wataionea bendera hofu kuu, asema Bwana, ambaye moto wake u katika Sayuni, na tanuru yake katika Yerusalemu.

Isaya 32

2 Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu. 3 Tena macho yao waonao hayatakuwa na kiwi, na masikio yao wasikiao yatasikiliza. 4 Tena moyo wa mtu mwenye hamaki utafahamu maarifa, na ndimi zao wenye kigugumizi zitakuwa tayari kunena sawasawa. 5 Mpumbavu hataitwa tena mwungwana, wala ayari hatasemwa kwamba ni karimu. 6 Maana mpumbavu atanena yaliyo upumbavu, na moyo wake utafanya maovu, ili kutenda hila na kusema yasiyo kweli juu ya Bwana, ili kuziacha nafsi za watu wenye njaa hazina kitu, na kukikomesha kinywaji chake mwenye kiu. 7 Tena vyombo vyake ayari ni vibaya; hutunga hila mbaya, ili kuwaangamiza wanyonge kwa maneno ya uongo, mtu mhitaji ajaposema maneno yenye haki. 8 Bali mwungwana huwaza mambo ya kiungwana, naye hushika sana mambo ya kiungwana. 9 Inukeni, enyi wanawake wenye raha, isikieni sauti yangu; enyi binti za watu msiokuwa na uangalifu, tegeni masikio yenu msikie matamko yangu. 10 Maana mtataabishwa siku kadha wa kadha zaidi ya mwaka, enyi wanawake mliojikinai; kwa sababu mavuno ya mizabibu yatakoma, wakati wa kuvuna vitu vya mashamba hautakuja. 11 Tetemekeni, enyi wanawake wenye raha; taabikeni, enyi msiokuwa na uangalifu; jivueni, jivueni nguo zenu kabisa, jivikeni viuno nguo za magunia. 12 Watajipiga vifua kwa ajili ya mashamba mazuri, kwa ajili ya mzabibu uliozaa sana. 13 Juu ya nchi ya watu wangu itamea michongoma na mibigili; naam, juu ya nyumba za furaha katika mji ulio na shangwe; 14 maana jumba la mfalme litaachwa; mji uliokuwa na watu wengi utakuwa hauna mtu; kilima na mnara utakuwa makao ya wanyama milele, furaha ya punda-mwitu, malisho ya makundi ya kondoo; 15 hata roho itakapomwagwa juu yetu kutoka juu; hata jangwa litakapokuwa shamba lizaalo sana; nalo shamba lizaalo sana litakapohesabiwa kuwa msitu. 16 Ndipo hukumu itakaa katika jangwa, na haki itakaa katika shamba lizaalo sana. 17 Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima. 18 Na watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu. 19 Lakini mvua ya mawe itakunya, wakati wa kuangushwa miti ya msituni; na huo mji utadhilika. 20 Heri ninyi mpandao mbegu kando ya maji yote, na kuiacha miguu ya ng'ombe na punda waende ko kote.

Isaya 33

2 Ee Bwana, uturehemu; tumekungoja wewe; uwe wewe mkono wetu kila asubuhi,na wokovu wetu pia wakati wa taabu. 3 Kabila za watu wamekimbia wakisikia kelele za fujo; mataifa wametawanyika ulipojiinua nafsi yako. 4 Na mateka yako yatakumbwa kama wadudu wakumbavyo, wataruka juu yake kama arukavyo nzige. 5 Bwana ametukuka; kwa maana anakaa juu; amejaza Sayuni hukumu na haki. 6 Nyakati zako zitakuwa nyakati za kukaa imara; za wokovu tele na hekima na maarifa; kumcha Bwana ni hazina yake ya akiba. 7 Angalia, mashujaa wao wanalia nje, wajumbe wa amani wanalia kwa uchungu. 8 Njia kuu zimeachwa, msafiri amekoma; ameyavunja maagano, ameidharau miji, hamjali mtu. 9 Nchi inaomboleza, na kulegea; Lebanoni imetahayarika na kunyauka; Sharoni imekuwa kama jangwa; Bashani na Karmeli zimepukutika majani. 10 Basi, sasa nitasimama; asema Bwana; sasa nitajiinua, sasa nitajitukuza. 11 Ninyi mtachukua mimba ya makapi, mtazaa majani makavu; pumzi yenu ni moto utakaowateketeza wenyewe. 12 Nao mataifa watakuwa kama kuchoma chokaa, kama miiba iliyokatika, iteketezwayo motoni. 13 Sikieni, ninyi mlio mbali, niliyoyatenda; na ninyi mlio karibu, kirini uweza wangu. 14 Wenye dhambi walio katika Sayuni wanaogopa; tetemeko limewashika wasiomcha Mungu; Ni nani kwetu sisi awezaye kukaa na moto ulao; ni nani kwetu sisi awezaye kukaa na moto uteketezao milele? 15 Ni yeye aendaye kwa haki, anenaye maneno ya adili; ni yeye anayedharau faida ipatikanayo kwa dhuluma; akung'utaye mikono yake asipokee rushwa; azibaye masikio yake asisikie habari za damu; afumbaye macho yake asitazame uovu. 16 Huyu ndiye atakayekaa juu; majabali ni ngome yake; atapewa chakula chake; maji yake hayatakoma. 17 Macho yako yatamwona mfalme katika uzuri wake, yataona nchi iliyoenea sana. 18 Moyo wako utatafakari hofu ile; Yuko wapi yeye aliyehesabu? Yuko wapi yeye aliyeupima ushuru? Yuko wapi yeye aliyeihesabu minara? 19 Hutawaona watu wale wakali; watu wa maneno magumu usiyoweza kuyafahamu; wenye lugha ya kigeni usiyoweza kuelewa nayo. 20 Angalia Sayuni, mji wa sikukuu zetu; macho yako yatauona Yerusalemu umekuwa kao la raha; hema isiyotanga-tanga; vigingi vyake havitang'olewa, wala kamba zake hazitakatika. 21 Bali huko Bwana atakuwa pamoja nasi, mwenye adhama; mahali penye mito mipana na vijito, pasipopita mashua na makasia yake; wala hapana merikebu ya vita itakayopita hapo. 22 Kwa maana Bwana ndiye mwamuzi wetu; Bwana ndiye mfanya sheria wetu; Bwana ndiye mfalme wetu; ndiye atakayetuokoa. 23 Kamba zako zimelegea; hawakuweza kukaza sana shina la mlingoti wao; hawakuweza kulikunjua tanga; ndipo mapato ya mateka yaligawanywa, hata wachechemeao walipata mateka. 24 Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.

Isaya 34

1 Karibuni, enyi mataifa, mpate kusikia; sikilizeni, enyi kabila za watu; dunia na isikie, nacho kiijazacho, ulimwengu na vitu vyote viutokavyo. 2 Maana Bwana ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote; amewaangamiza kabisa, amewatoa waende kuchinjwa. 3 Watu wao waliouawa watatupwa nje, na uvundo wa maiti zao utapaa juu, na milima itayeyushwa kwa damu yao. 4 Na jeshi lote la mbinguni litafumuliwa, na mbingu zitakunjwa kama karatasi, na jeshi lao lote litanyauka kama vile jani la mzabibu linyaukavyo na kupukutika, na kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika. 5 Maana upanga wangu umekunywa na kushiba mbinguni; tazama, utashukia Edomu, na juu ya watu wa laana yangu, ili kuwahukumu. 6 Upanga wa Bwana umeshiba damu, umenona kwa unono, kwa damu ya wana-kondoo na mbuzi, kwa mafuta ya figo za kondoo waume; maana Bwana ana dhabihu huko Bozra, machinjo makubwa katika nchi ya Edomu. 7 Na nyati watatelemka pamoja nao, na mahasai pamoja na mafahali, na nchi yao italewa kwa damu, na mavumbi yake yatanoneshwa kwa shahamu. 8 Maana ni siku ya kisasi cha Bwana, mwaka wa malipo, ili kushindania Sayuni. 9 Na vijito vyake vitageuzwa kuwa lami, na mavumbi yake yatageuzwa kuwa kiberiti, na ardhi yake itakuwa lami iwakayo. 10 Haitazimwa mchana wala usiku, moshi wake utapaa milele; tangu kizazi hata kizazi itakuwa ukiwa; hapana mtu atakayepita kati yake milele na milele. 11 Kaati na nungu wataimiliki, bundi na kunguru watakaa huko, naye atanyosha juu yake kamba ya ukiwa na timazi ya utupu. 12 Watawaitia wakuu wake ufalme, lakini hawatakuwapo; wakuu wake wote wamekuwa si kitu. 13 Miiba itamea majumbani mwake, upupu na mbigili ndani ya maboma yake; nayo itakuwa kao la mbweha, na ua la mbuni. 14 Na hayawani wa nyikani watakutana na mbwa-mwitu, na beberu anamwita mwenziwe; naam, babewatoto anakaa huko na kujipatia raha. 15 Huko pili atafanya kioto chake na kuzaa na kuotamia, na kukusanya watoto wake katika kivuli chake; naam, huko watakusanyika tai, kila mmoja na mwenzake. 16 Tafuteni katika kitabu cha Bwana mkasome; hapana katika hao wote atakayekosa kuwapo, hapana mmoja atakayemkosa mwenzake; kwa maana kinywa changu kimeamuru, na roho yake imewakusanya. 17 Naye amewapigia kura, na mkono wake umewagawanyia kwa kamba; wataimiliki hata milele, watakaa ndani yake kizazi hata kizazi.

Isaya 35

1 Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. 2 Litachanua maua mengi, na kufurahi, naam, kwa shangwe na kuimba; litapewa uzuri wa Lebanoni, utukufu wa Karmeli na Sharoni; watauona utukufu wa Bwana, ukuu wa Mungu wetu. 3 Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu, yafanyeni imara magoti yaliyolegea. 4 Waambieni walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope; tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi. 5 Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. 6 Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba; maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. 7 Na mchanga ung'aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji; katika makao ya mbweha, walipokuwa wamelala, patakuwa na majani, pamoja na mianzi na manyasi. 8 Na hapo patakuwa na njia kuu, na njia, nayo itaitwa, Njia ya utakatifu; wasio safi hawatapita juu yake; bali itakuwa kwa ajili ya watu hao; wasafirio, wajapokuwa wajinga, hawatapotea katika njia hiyo. 9 Hapo hapatakuwa na simba, wala mnyama mkali hatapanda juu yake; hawataonekana hapo; bali waliokombolewa watakwenda katika njia hiyo. 10 Na hao waliokombolewa na Bwana watarudi, watafika Sayuni wakiimba; na furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao; nao watapata kicheko na furaha, huzuni na kuugua zitakimbia.

Isaya 36

2 Mfalme wa Ashuru akamtuma amiri toka Lakishi hata Yerusalemu,kwa mfalme Hezekia,pamoja na jeshi kubwa. Naye akasimama karibu na mfereji wa birika ya juu,iliyo katika njia kuu ya kuuendea uwanda wa dobi. 3 Wakamtokea Eliakimu, mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba ya mfalme, na Shebna, mwandishi, na Yoa, mwana wa Asafu, mwenye kuandika tarehe. 4 Yule amiri akawaambia, Haya, mwambieni Hezekia, kwamba mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru, asema hivi, Ni tumaini gani hili unalolitumainia? 5 Nasema, mashauri yako, na nguvu zako kwa vita, ni maneno yasiyo na maana; basi, unamtumaini nani hata ukaniasi mimi? 6 Tazama, unaitumainia fimbo ya mwanzi huu uliopondeka, yaani, Misri, ambayo, mtu akitegemea juu yake, humwingia mkononi na kumchoma; ndivyo alivyo Farao, mfalme wa Misri, kwa wote wamtumainio. 7 Lakini ukiniambia, Tunamtumaini Bwana, Mungu wetu, je! Si yeye ambaye Hezekia ameondoa mahali pake mlimoinuka, na madhabahu zake, akawaambia watu wa Yuda na Yerusalemu, Sujuduni mbele ya madhabahu hii? 8 Basi sasa, tafadhali mpe bwana wangu, mfalme wa Ashuru, dhamana, nami nitakupa farasi elfu mbili, ikiwa wewe kwa upande wako waweza kupandisha watu juu yao. 9 Wawezaje, basi, kurudisha nyuma uso wa akida mmoja wa watumishi walio wadogo wa bwana wangu, na kuitumainia Misri upewe magari na farasi? 10 Je! Nimepanda mimi, ili kupigana na mahali hapa na kupaangamiza, bila shauri la Bwana? Bwana ndiye aliyeniambia, Panda upigane na nchi hii na kuiangamiza. 11 Ndipo Eliakimu, mwana wa Hilkia, na Shebna, na Yoa, wakamwambia yule amiri, Tafadhali, sema na watumishi wako kwa lugha ya Kiashuri; maana tunaifahamu; wala usiseme nasi kwa lugha ya Kiyahudi, masikioni mwa watu wote walio ukutani. 12 Lakini yule amiri akawaambia, Je! Bwana wangu amenituma kwa bwana wako, na kwako wewe, niseme maneno haya? Hakunituma kwa watu hawa walio ukutani, ili wale mavi yao wenyewe na kunywa mkojo wao pamoja nanyi? 13 Kisha yule amiri akasimama akalia kwa sauti kuu kwa lugha ya Kiyahudi, akisema, Lisikieni neno la mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru. 14 Mfalme asema hivi; Hezekia asiwadanganye, kwa maana hataweza kuwaokoa; 15 wala msimwache Hezekia kuwatia moyo wa kumtumaini Bwana; akisema, Bwana bila shaka atatuokoa, mji huu hautatiwa katika mkono wa mfalme wa Ashuru. 16 Msimsikilize Hezekia; maana mfalme wa Ashuru asema hivi, Fanyeni suluhu na mimi, mkatoke mnijie, mkale kila mtu matunda ya mzabibu wake na matunda ya mtini wake, mkanywe kila mmoja maji ya birika yake mwenyewe; 17 hata nije nikawachukue mpaka nchi iliyo kama nchi yenu wenyewe, nchi ya nafaka na divai, nchi ya mkate na mashamba ya mizabibu. 18 Jihadharini, asije Hezekia akawadanganya, akisema, Bwana atatuokoa. Je! Yuko mungu mmoja wa mataifa aliyewaokoa watu wake na mkono wa mfalme wa Ashuru? 19 Wako wapi miungu ya Hamathi na ya Arpadi? Wako wapi miungu ya Sefarvaimu? Je! Wameiokoa Samaria na mkono wangu? 20 Katika miungu yote ya nchi hizi ni nani waliookoa nchi yao na mkono wangu, hata Bwana auokoe Yerusalemu na mkono wangu? 21 Lakini watu wakanyamaza kimya; wala hawakumjibu hata neno moja; maana ilikuwa amri ya mfalme, kwamba, Msimjibu neno. 22 Ndipo Eliakimu, mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba ya mfalme, na Shebna, mwandishi, na Yoa, mwana wa Asafu mwenye kuandika tarehe, wakaenda kwa Hezekia, na nguo zao zimeraruliwa, wakamwambia Hezekia maneno ya yule amiri.

Isaya 37

1 Ikawa mfalme Hezekia aliposikia hayo, alizirarua nguo zake, akajivika nguo za magunia, akaingia katika nyumba ya Bwana. 2 Akamtuma Eliakimu aliyekuwa msimamizi wa nyumba yake na Shebna, mwandishi, na wazee wa makuhani, wamejivika nguo za magunia, waende kwa Isaya nabii, mwana wa Amozi. 3 Wakamwambia, Hezekia asema hivi, Siku hii ni siku ya dhiki, na aibu, na matukano; maana watoto wa tayari kuzaliwa, wala hapana nguvu za kuwazaa. 4 Yamkini Bwana, Mungu wako, atayasikia maneno ya huyo amiri ambaye mfalme wa Ashuru, bwana wake, amemtuma ili amtukane Mungu aliye hai; na Bwana, Mungu wako atayakemea maneno aliyoyasikia; basi, inua dua yako kwa ajili ya mabaki yaliyobakia. 5 Basi, watumishi wa mfalme Hezekia wakaenda kwa Isaya. 6 Isaya akawaambia, Mwambieni bwana wenu maneno haya; Bwana asema hivi, Usiyaogope maneno uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mfalme wa Ashuru wamenitukana. 7 Tazama, nitatia roho ndani yake, naye atasikia kivumi, na kurudi hata nchi yake mwenyewe, nami nitamwangusha kwa upanga katika nchi yake mwenyewe. 8 Basi yule amiri akarudi, akamkuta mfalme wa Ashuru anafanya vita juu ya Libna; kwa maana alikuwa amesikia ya kwamba ameondoka, akaacha Lakishi. 9 Naye alisikia habari ya Tirhaka, mfalme wa Kushi, ya kwamba, Ametoka ili kupigana nawe; naye aliposikia hayo, akatuma wajumbe kwa Hezekia, kusema, 10 Mwambieni Hezekia, mfalme wa Yuda, maneno haya, mkisema, Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru. 11 Tazama, umesikia habari ya mambo yote, ambayo wafalme wa Ashuru wamezitenda nchi zote, kwa kuziangamiza kabisa je! Utaokoka wewe? 12 Je! Miungu ya mataifa, ambao baba zangu waliwaangamiza, wamewaokoa? Gozani, na Harani, na Resefu, na wana wa Adini waliokuwa katika Telasari? 13 Yuko wapi mfalme wa Hamathi, na mfalme wa Arpadi, na mfalme wa mji wa Sefarvaimu, wa Hena, na wa Iva? 14 Basi Hezekia akaupokea waraka katika mikono ya wale wajumbe, akausoma; kisha Hezekia akapanda, akaingia katika nyumba ya Bwana, akaukunjua mbele za Bwana. 15 Hezekia akamwomba Bwana, akisema, 16 Ee Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia. Wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi. 17 Tega sikio lako, Bwana, usikie; funua macho yako, Bwana, uone; uyasikie maneno ya Senakeribu, aliyopeleka ili kumtukana Mungu aliye hai. 18 Ni kweli, Bwana, wafalme wa Ashuru wameziharibu nchi zote, na mashamba yao, 19 na kuwatupa miungu yao motoni; kwa maana hao hawakuwa miungu, bali kazi ya mikono ya wanadamu; walikuwa miti na mawe, ndiyo sababu wakawaharibu. 20 Basi sasa, Bwana, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe Bwana, wewe peke yako. 21 Ndipo Isaya, mwana wa Amozi, akapeleka ujumbe kwa Hezekia, akisema, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa kuwa umeniomba juu ya Senakeribu, mfalme wa Ashuru, 22 tamko alilolitamka Bwana katika habari zake ndilo hili; Bikira, binti Sayuni, anakudharau, anakudhihaki sana; binti Yerusalemu anatikisa kichwa chake juu yako. 23 Ni nani uliyemshutumu na kumtukana? Umeinua sauti yako juu ya nani, na kuinua macho yako juu? Juu ya Mtakatifu wa Israeli. 24 Umemshutumu Bwana kwa watumishi wako, kwa kuwa umesema, Kwa wingi wa magari yangu nimepanda juu ya vilele vya milima, mpaka mahali pa ndani ya Lebanoni; nami nitaikata mierezi yake mirefu, na misunobari yake mizuri, nami nitaingia ndani ya mahali pake palipoinuka, palipo mbali sana, msitu wa shamba lake lizaalo sana. 25 Nimechimba na kunywa maji, na kwa nyayo za miguu yangu nitaikausha mito yote ya Misri. 26 Je! Hukusikia? Ni mimi niliyeyatenda hayo tokea zamani, na kuyafanya tokea siku za kale; nikayatimiza sasa, iwe kazi yako kuangamiza miji yenye boma, ikawe chungu na magofu. 27 Ndiyo sababu wenyeji wao wakawa hawana nguvu, na kufadhaika, na kuhangaika, wakawa kama majani ya mashamba, kama miche mibichi, kama majani juu ya dari, kama shamba la ngano kabla haijaiva. 28 Lakini nakujua, kuketi kwako, na kutoka kwako, na kuingia kwako; na ghadhabu yako uliyonighadhibikia. 29 Kwa sababu ya kunighadhibikia kwako, na kwa sababu kutakabari kwako kumefika masikioni mwangu, nitatia kulabu yangu katika pua yako, na hatamu yangu midomoni mwako, nami nitakurudisha kwa njia ile ile uliyoijia. 30 Na kwako wewe dalili ndiyo hii; mwaka huu mtakula vitu vimeavyo vyenyewe; na mwaka wa pili mtakula mazao ya mbegu za vitu hivyo; na mwaka wa tatu pandeni mbegu, kavuneni; mkapande mizabibu katika mashamba, mkale matunda yake. 31 Na mabaki yaliyookoka, yaliyobakia ya nyumba ya Yuda, yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu. 32 Maana katika Yerusalemu yatatoka mabaki, nao watakaookoka katika mlima Sayuni; wivu wa Bwana wa majeshi utatimiza mambo hayo. 33 Basi, Bwana asema hivi katika habari za mfalme wa Ashuru, Yeye hataingia ndani ya mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hatakuja mbele yake kwa ngao, wala hatajenga boma juu yake. 34 Njia ile ile aliyoijia, kwa njia hiyo atarudi zake, wala hataingia ndani ya mji huu; asema Bwana. 35 Nami nitaulinda mji huu, niuokoe kwa ajili yangu mwenyewe, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu. 36 Basi malaika wa Bwana alitoka, akaua watu mia na themanini na tano elfu katika kituo cha Waashuri, na watu walipoamka asubuhi na mapema, kumbe, hao walikuwa maiti wote pia. 37 Basi Senakeribu, mfalme wa Ashuru akaenda zake, akarudi Ninawi, akakaa huko. 38 Ikawa alipokuwa akiabudu katika nyumba ya Nisroki, mungu wake, Adrameleki na Shareza, wanawe, wakampiga kwa upanga; wakakimbilia nchi ya Ararati; naye Esar-hadoni, mwanawe, akamiliki badala yake.

Isaya 38

1 Siku hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. 2 Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana, 3 akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. 4 Ikawa, neno la Bwana likamjia Isaya, kusema, 5 Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako, asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. 6 Nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu. 7 Jambo hili liwe ishara kwako, itokayo kwa Bwana, ya kuwa Bwana atalitimiza jambo hili alilolisema; 8 Tazama, nitakirudisha nyuma kivuli madaraja kumi, ambayo kilishuka juu ya duara ya Ahazi kwa sababu ya jua. Basi jua likarudi madaraja kumi katika hiyo duara, ambayo limekwisha kushuka. 9 Haya ndiyo maandiko ya Hezekia, mfalme wa Yuda, alipokuwa hawezi, naye akapona ugonjwa wake. 10 Nalisema, Katika usitawi wa siku zangu nitakwenda kuingia malango ya kuzimu; Nimenyimwa mabaki ya miaka yangu. 11 Nalisema, Sitamwona Bwana, yeye Bwana, katika nchi ya walio hai; Sitamwona mwanadamu tena pamoja na hao wakaao duniani. 12 Kao langu limeondolewa kabisa, limechukuliwa kama hema ya mchungaji; Nimekunja maisha yangu kama mfumaji; atanikatilia mbali na kitanda cha mfumi; Tangu mchana hata usiku wanimaliza. 13 Nalijituliza hata asubuhi; kama simba, aivunja mifupa yangu yote; Tangu mchana hata usiku wanimaliza. 14 Kama mbayuwayu au korongo ndivyo nilivyolia; Naliomboleza kama hua; macho yangu yamedhoofu kwa kutazama juu; Ee Bwana, nimeonewa, na uwe mdhamini wangu. 15 Niseme nini? Yeye amenena nami, na yeye mwenyewe ametenda hayo; Nitakwenda polepole miaka yangu yote, kwa sababu ya uchungu wa nafsi yangu. 16 Ee Bwana, kwa mambo hayo watu huishi; Na uhai wa roho yangu u katika hayo yote; Kwa hiyo uniponye na kunihuisha. 17 Tazama; nalikuwa na uchungu mwingi kwa ajili ya amani yangu; Lakini kwa kunipenda umeniokoa na shimo la uharibifu; Kwa maana umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako. 18 Kwa kuwa kuzimu hakuwezi kukusifu; mauti haiwezi kukuadhimisha; Wale washukao shimoni hawawezi kuitarajia kweli yako. 19 Aliye hai, naam, aliye hai, ndiye atakayekusifu, kama mimi leo; Baba atawajulisha watoto kweli yako. 20 Bwana yu tayari kunipa wokovu. Basi, kwa vinubi tutaziimba nyimbo zangu, Siku zote za maisha yetu nyumbani mwa Bwana. 21 Maana Isaya amesema, Na watwae mkate wa tini, wakauweke juu ya jipu, naye atapona. 22 Tena Hezekia alikuwa amesema, Iko ishara gani ya kunionyesha ya kuwa nitapanda niingie nyumbani mwa Bwana?

Isaya 39

1 Wakati huo Merodaki-baladani, mwana wa Baladani, mfalme wa Babeli, alipeleka barua na zawadi kwa Hezekia; kwa maana amepata habari kwamba amekuwa hawezi, na kwamba amepona. 2 Hezekia akawafurahia, akawaonyesha nyumba yake yenye vitu vyake vya thamani, fedha na dhahabu, na manukato, na marhamu ya thamani, na nyumba yote yenye silaha zake za vita, na vitu vyote vilivyoonekana katika hazina zake; hapakuwa na kitu nyumbani mwake wala katika ufalme wake asichowaonyesha. 3 Ndipo Isaya nabii akamwendea mfalme Hezekia, akamwambia, Watu hawa walisema nini? Nao wametoka wapi kuja kwako? Hezekia akasema, Wametoka katika nchi iliyo mbali, wakaja kwangu toka Babeli. 4 Ndipo akasema, Wameona nini katika nyumba yako? Hezekia akajibu, Wameviona vitu vyote vilivyomo nyumbani mwangu; hapana kitu katika hazina zangu nisichowaonyesha. 5 Ndipo Isaya akamwambia Hezekia, Basi, lisikie neno la Bwana wa majeshi. 6 Tazama, siku zinakuja, ambazo vitu vyote vilivyomo nyumbani mwako, na hivyo vilivyowekwa akiba na baba zako hata leo, vitachukuliwa mpaka Babeli; hapana kitu cho chote kitakachosalia; asema Bwana. 7 Na baadhi ya wana wako utakaowazaa, watakaotoka kwako, watawachukulia mbali; nao watakuwa matowashi katika jumba la mfalme wa Babeli. 8 Ndipo Hezekia akamwambia Isaya, Neno la Bwana ulilolinena ni jema. Tena akamwambia, Maana itakuwapo amani na kweli katika siku zangu mimi.

Isaya 40

1 Watulizeni mioyo, watulizeni mioyo, watu wangu, asema Mungu wenu. 2 Semeni na moyo wa Yerusalemu, kauambieni kwa sauti kuu ya kwamba vita vyake vimekwisha, uovu wake umeachiliwa; kwa kuwa amepokea kwa mkono wa Bwana adhabu maradufu kwa dhambi zake zote. 3 Sikiliza, ni sauti ya mtu aliaye, Itengenezeni nyikani njia ya Bwana; Nyosheni jangwani njia kuu kwa Mungu wetu. 4 Kila bonde litainuliwa, Na kila mlima na kilima kitashushwa; Palipopotoka patakuwa pamenyoka, Na palipoparuza patasawazishwa; 5 Na utukufu wa Bwana utafunuliwa, Na wote wenye mwili watauona pamoja; Kwa kuwa kinywa cha Bwana kimenena haya. 6 Sikiliza, ni sauti ya mtu asemaye, Lia! Nikasema, Nilie nini? Wote wenye mwili ni majani, Na wema wake wote ni kama ua la kondeni; 7 Majani yakauka, ua lanyauka; Kwa sababu pumzi ya Bwana yapita juu yake. Yakini watu hawa ni majani. 8 Majani yakauka, ua lanyauka; Bali neno la Mungu wetu litasimama milele. 9 Wewe uuhubiriye Sayuni habari njema, Panda juu ya mlima mrefu; Wewe uuhubiriye Yerusalemu habari njema, Paza sauti kwa nguvu; Paza sauti yako, usiogope; Iambie miji ya Yuda, Tazameni, Mungu wenu. 10 Tazameni, Bwana Mungu atakuja kama shujaa, Na mkono wake ndio utakaomtawalia; Tazameni, thawabu yake i pamoja naye, Na ijara yake i mbele zake. 11 Atalilisha kundi lake kama mchungaji, Atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; Na kuwachukua kifuani mwake, Nao wanyonyeshao atawaongoza polepole. 12 Ni nani aliyeyapima maji kwa konzi ya mkono wake, na kuzikadiri mbingu kwa shubiri, na kuyashika mavumbi ya dunia katika pishi, na kuipima milima kwa uzani, na vilima kama kwa mizani? 13 Ni nani aliyemwongoza roho ya Bwana, na kumfundisha kwa kuwa mshauri wake? 14 Alifanya shauri na nani, ni nani aliyemwelimisha na kumfunza njia ya hukumu, na kumfunza maarifa, na kumwonyesha njia ya fahamu? 15 Tazama, mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani; tazama, yeye huvinyanyua visiwa kama ni kitu kidogo sana. 16 Lebanoni nayo hautoshi kwa kuni, wala wanyama wake hawatoshi kwa kafara. 17 Mataifa yote huwa kama si kitu mbele zake; huhesabiwa kwake kuwa duni ya si kitu, na ubatili. 18 Basi, mtamlinganisha Mungu na nani? Au mtamfananisha na mfano wa namna gani? 19 Sanamu fundi mmoja huiyeyusha, na mfua dhahabu huifunika dhahabu, huifulia mikufu ya fedha. 20 Yeye aliye maskini sana hata hawezi kutoa sadaka ya namna hii, huchagua mti usiooza, hujitafutia fundi mstadi wa kusimamisha sanamu ya kuchonga isiyoweza kutikisika. 21 Je! Hamkujua? Hamkusikia? Hamkuambiwa tokea mwanzo? Hamkufahamu tangu kuwekwa misingi ya dunia? 22 Yeye ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia, na hao wanaokaa ndani yake huwa kama panzi; yeye ndiye azitandazaye mbingu kama pazia na kuzikunjua kama hema ya kukaliwa; 23 ndiye awatanguaye wakuu, na kuwabatilisha waamuzi wa dunia. 24 Naam, hawakupandwa; hawakutiwa katika ardhi kama mbegu; naam, shina lao halikutia mizizi katika ardhi; tena awapuzia tu, wakanyauka, upepo wa kisulisuli wawaondoa kama mabua makavu. 25 Mtanifananisha na nani, basi, nipate kuwa sawa naye? Asema yeye aliye Mtakatifu. 26 Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake. 27 Mbona unasema, Ee Yakobo, mbona unanena, Ee Israeli, Njia yangu imefichwa, Bwana asiione, na hukumu yangu imempita Mungu wangu asiiangalie? 28 Je! Wewe hukujua? Hukusikia? Yeye Mungu wa milele, Bwana, Muumba miisho ya dunia, hazimii, wala hachoki; akili zake hazichunguziki. 29 Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. 30 Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; 31 bali wao wamngojeao Bwana watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.

Isaya 41

1 Nyamazeni mbele zangu, enyi visiwa, na mataifa wajipatie nguvu mpya; na waje karibu wakanene; na tukaribiane pamoja kwa hukumu. 2 Ni nani aliyemwinua mmoja atokaye mashariki, ambaye katika haki amemwita mguuni pake? Ampa mataifa mbele yake, na kumtawaza juu ya wafalme; awatoa wawe kama mavumbi kwa upanga wake, kama makapi yaliyopeperushwa kwa upinde wake. 3 Awafuatia, apita salama hata kwa njia asiyoikanyaga kamwe kwa miguu yake. 4 Ni nani aliyetenda na kufanya jambo hilo, aviitaye vizazi tangu mwanzo? Mimi, Bwana, wa kwanza na wa mwisho, mimi ndiye. 5 Visiwa vimeona, vikaogopa; ncha za dunia zilitetemeka; walikaribia, walikuja. 6 Wakasaidiana, kila mtu na mwenzake, kila mtu akamwambia ndugu yake; Uwe na moyo mkuu. 7 Seremala akamtia moyo mfua dhahabu, na yeye alainishaye kwa nyundo akamhimiza yule apigaye fuawe, akiisifu kazi ya kuunga, akisema, Ni kazi njema; naye akaikaza kwa misumari isitikisike. 8 Nawe, Israeli, mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu; 9 wewe niliyekushika toka miisho ya dunia, na kukuita toka pembe zake, nikikuambia, Wewe u mtumishi wangu; nimekuchagua wala sikukutupa; 10 usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu. 11 Tazama, wote walioona hasira juu yako watatahayarika na kufadhaika; watu washindanao nawe watakuwa si kitu, na kuangamia. 12 Utawatafuta wala hutawaona wale wapiganao nawe; watakuwa si kitu; watakuwa kama kitu kisichokuwa, wale waliofanya vita juu yako. 13 Kwa maana mimi, Bwana, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia. 14 Usiogope, Yakobo uliye mdudu, nanyi watu wa Israeli; mimi nitakusaidia, asema Bwana, na mkombozi wako ni Mtakatifu wa Israeli. 15 Tazama, nitakufanya kuwa chombo kikali kipya cha kupuria, chenye meno; utaifikicha milima, na kuisaga; nawe utafanya vilima kuwa kama makapi. 16 Utawapepeta, na upepo utawapeperusha; upepo wa kisulisuli utawatawanya; nawe utamfurahia Bwana, utajitukuza katika Mtakatifu wa Israeli. 17 Maskini na wahitaji wanatafuta maji, wala hapana; ndimi zao zimekauka kwa kiu; mimi, Bwana, nitawasikia, mimi, Mungu wa Israeli, sitawaacha. 18 Nitafunua vijito vya maji juu ya vilima, na chemchemi katikati ya mabonde; nitageuza jangwa kuwa ziwa la maji, na mahali pakavu kuwa vijito vya maji. 19 Nitapanda katika jangwa mwerezi, mshita, mhadasi, na mbono; nitatia katika nyika mberoshi, mtidhari, na mteashuri pamoja; 20 ili waone, na kujua, wakafikiri, na kufahamu pamoja, ya kuwa mkono wa Bwana ndio uliofanya jambo hilo. Mtakatifu wa Israeli ndiye aliyeliumba. 21 Haya, leteni maneno yenu, asema Bwana; toeni hoja zenu zenye nguvu, asema mfalme wa Yakobo. 22 Wayatangaze na kutujulisha yatakayokuwa; watuonyeshe mambo ya zamani, ni mambo gani, tukapate kuyatia moyoni, tukajue mwisho wake; au wamdhihirishie yatakayotokea baadaye. 23 Tujulisheni yatakayokuwa baadaye, nasi tutakiri ya kuwa ninyi ni miungu; naam, tendeni mema au tendeni mabaya, ili tujipime, tukaone pamoja. 24 Tazameni, ninyi si kitu, tena kazi yenu si kitu; awachaguaye ninyi ni chukizo. 25 Nimemwinua mtu toka kaskazini, naye amekuja; toka maawio ya jua amekuja anitajaye jina langu; naye atawajilia maliwali kama akanyagaye matope, na kama mfinyanzi afinyangaye udongo. 26 Ni nani aliyeihubiri habari tokea mwanzo, tupate kuijua? Na tokea zamani, tupate kusema, Yeye ni mwenye haki? Naam, hapana hata mmoja aliyetujulisha; naam, hapana hata mmoja aliyetuonyesha; naam, hapana hata mmoja aliyesikia maneno yenu. 27 Mimi kwanza nitauambia Sayuni, Tazama; hawa ndio; nami nitampa Yerusalemu mletaji wa habari njema. 28 Na nitazamapo, hapana mtu, hata katika watu hao hapana mshauri mmoja, ambaye, nikimwuliza, aweza kunijibu neno. 29 Tazama, hao wote ni ubatili; kazi zao si kitu; sanamu zao ni upepo na fujo.

Isaya 42

1 Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. 2 Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. 3 Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli. 4 Hatazimia, wala hatakata tamaa, hata atakapoweka hukumu duniani; na visiwa vitaingojea sheria yake. 5 Mungu Bwana anena, yeye aliyeziumba mbingu, na kuzitanda; yeye aliyeitandaza nchi na mazao yake; yeye awapaye pumzi watu walio juu yake; yeye awapaye roho wao waendao ndani yake. 6 Mimi, Bwana, nimekuita katika haki, nami nitakushika mkono, na kukulinda, na kukutoa uwe agano la watu, na nuru ya mataifa; 7 kuyafunua macho ya vipofu, kuwatoa gerezani waliofungwa, kuwatoa wale walioketi gizani katika nyumba ya kufungwa. 8 Mimi ni Bwana; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu. 9 Tazama, mambo ya kwanza yamekuwa, nami nayahubiri mambo mapya; kabla hayajatokea nawapasheni habari zake. 10 Mwimbieni Bwana wimbo mpya, Na sifa zake tokea mwisho wa dunia; Ninyi mshukao baharini, na vyote vilivyomo, Na visiwa, nao wakaao humo. 11 Jangwa na miji yake na ipaze sauti zao, Vijiji vinavyokaliwa na Kedari; Na waimbe wenyeji wa Sela, Wapige kelele toka vilele vya milima. 12 Na wamtukuze Bwana, Na kutangaza sifa zake visiwani. 13 Bwana atatokea kama shujaa; Ataamsha wivu kama mtu wa vita; Atalia, naam, atapiga kelele; Atawatenda adui zake mambo makuu. 14 Siku nyingi nimenyamaza kimya; nimenyamaza, nikajizuia; sasa nitapiga kelele kama mwanamke aliye katika kuzaa; nitaugua na kutweta pamoja. 15 Nitaharibu milima na vilima, nitavikausha vyote vimeavyo; nitaifanya mito ya maji kuwa visiwa, na kuyakausha maziwa ya maji. 16 Nitawaleta vipofu kwa njia wasiyoijua; katika mapito wasiyoyajua nitawaongoza; nitafanya giza kuwa nuru mbele yao; na mahali palipopotoka kuwa pamenyoka. Haya nitayatenda, wala sitawaacha. 17 Watarudishwa nyuma, wataaibishwa sana, hao wanaotumainia sanamu za mawe, na kuziambia sanamu za madini, Ninyi ndinyi miungu yetu. 18 Sikilizeni, enyi viziwi; tazameni, enyi vipofu, mpate kuona. 19 Ni nani aliye kipofu, ila mtumishi wangu? Au aliye kiziwi, kama mjumbe wangu nimtumaye? Ni nani aliye kipofu, kama yeye aliye na amani? Naam, kipofu kama mtumishi wa Bwana? 20 Unaona mambo mengi, lakini huyatii moyoni; masikio yake ya wazi, lakini hasikii. 21 Bwana akapendezwa, kwa ajili ya haki yake, kuitukuza sheria, na kuiadhimisha. 22 Lakini watu hawa ni watu walioibiwa na kutekwa; wote wamenaswa katika mashimo, wamefichwa katika magereza; wamekuwa mawindo, wala hapana aokoaye; wamekuwa mateka, wala hapana asemaye, Rudisha. 23 Ni nani miongoni mwenu atakayetega sikio lake kuyasikia hayo? Atakayesikiliza na kusikia kwa wakati ujao? 24 Ni nani aliyemtoa Yakobo awe mateka, aliyemtia Israeli katika mikono ya wanyang'anyi? Si yeye, Bwana? Yeye tuliyemkosa, ambaye hawakutaka kwenda katika njia zake, wala hawakuitii sheria yake. 25 Kwa sababu hiyo alimwaga ukali wa hasira yake juu yake, na nguvu za vita; ukawasha moto wa kumzunguka pande zote, wala hakujua; ukamteketeza, wala hakuyatia hayo moyoni mwake.

Isaya 43

1 Lakini sasa, Bwana aliyekuhuluku, Ee Yakobo, yeye aliyekuumba, Ee Israeli, asema hivi, Usiogope, maana nimekukomboa; nimekuita kwa jina lako, wewe u wangu. 2 Upitapo katika maji mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha; uendapo katika moto, hutateketea; wala mwali wa moto hautakuunguza. 3 Maana mimi ni Bwana, Mungu wako; Mtakatifu wa Israeli, mwokozi wako, nimetoa Misri kuwa ukombozi wako; nimetoa Kushi na Seba kwa ajili yako. 4 Kwa kuwa ulikuwa wa thamani machoni pangu, na mwenye kuheshimiwa, nami nimekupenda; kwa sababu hiyo nitatoa watu kwa ajili yako; na kabila za watu kwa ajili ya maisha yako. 5 Usiogope; maana mimi ni pamoja nawe; nitaleta wazao wako toka mashariki, nitakukusanya toka magharibi; 6 nitaiambia kaskazi, Toa; nayo kusi, Usizuie; waleteni wana wangu kutoka mbali, na binti zangu kutoka miisho ya dunia. 7 Kila mmoja aliyeitwa kwa jina langu, niliyemwumba kwa ajili ya utukufu wangu; mimi nimemwumba, naam, mimi nimemfanya. 8 Walete vipofu walio na macho, na viziwi walio na masikio. 9 Na wakusanyike mataifa yote, kabila zote wakutanike; ni nani miongoni mwao awezaye kuhubiri neno hili, na kutuonyesha mambo ya zamani? Na walete mashahidi wao, wapate kuhesabiwa kuwa na haki; au na wasikie, wakaseme, Ni kweli. 10 Ninyi ni mashahidi wangu, asema Bwana, na mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine. 11 Mimi, naam, mimi, ni Bwana, zaidi yangu mimi hapana mwokozi. 12 Nimetangaza habari, nimeokoa, nimeonyesha, na hapakuwa mungu wa kigeni kati yenu; kwa sababu hiyo ninyi ni mashahidi wangu, asema Bwana, nami ni Mungu. 13 Naam, tangu siku ya leo, mimi ndiye; wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu; mimi nitatenda kazi, naye ni nani awezaye kuizuia? 14 Bwana, Mkombozi wenu, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi; Kwa ajili yenu nimetuma ujumbe Babeli nami nitawashusha wote mfano wa wakimbizi, naam, Wakaldayo, katika merikebu zao walizozifurahia. 15 Mimi ni Bwana, Mtakatifu wenu, Muumba wa Israeli, mfalme wenu. 16 Bwana asema hivi, yeye afanyaye njia katika bahari; na mahali pa kupita katika maji yenye nguvu; 17 atoaye gari na farasi, jeshi la askari na uwezo; wamelala, hawataondoka; wametoweka, wamezimwa mfano wa utambi. 18 Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani. 19 Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani. 20 Wanyama wa kondeni wataniheshimu, mbweha pia na mbuni; kwa sababu nimewapa maji jangwani, na mito nyikani, ili kuwanywesha watu wangu, wateule wangu; 21 watu wale niliojiumbia nafsi yangu, ili wazitangaze sifa zangu. 22 Lakini hukuniita, Ee Yakobo, bali umechoka nami, Ee Israeli. 23 Hukuniletea wana-kondoo kuwa kafara zako, wala hukuniheshimu kwa dhabihu zako. Sikukutumikisha kwa matoleo, wala sikukuchosha kwa ubani. 24 Hukuninunulia manukato kwa fedha, wala hukunishibisha kwa mafuta ya sadaka zako; bali umenitumikisha kwa dhambi zako, umenichosha kwa maovu yako. 25 Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka dhambi zako. 26 Unikumbushe, na tuhojiane; eleza mambo yako, upate kupewa haki yako. 27 Baba yako wa kwanza alifanya dhambi, na wakalimani wako wameniasi. 28 Kwa hiyo nitawatia unajisi wakuu wa patakatifu, nami nitamfanya Yakobo kuwalaani, na Israeli kuwa tukano.

Isaya 44

1 Lakini sikia sasa, Ee Yakobo, mtumishi wangu; na Israeli, niliyekuchagua; 2 Bwana, aliyekufanya, na kukuumba toka tumboni, yeye atakayekusaidia, asema hivi; Usiogope, Ee Yakobo, mtumishi wangu; na wewe, Yeshuruni, niliyekuchagua. 3 Kwa maana nitamimina maji juu yake aliye na kiu, na vijito vya maji juu ya mahali pakavu; nitamwaga roho yangu juu ya wazao wako, na baraka yangu juu yao utakaowazaa; 4 nao watatokea katika manyasi, kama mierebi karibu na mifereji ya maji. 5 Mmoja atasema, Mimi ni wa Bwana; na mwingine atajiita kwa jina la Yakobo; na mwingine ataandika juu ya mkono wake, Kwa Bwana, na kujiita kwa jina la Israeli. 6 Bwana, Mfalme wa Israeli, Mkombozi wako, Bwana wa majeshi, asema hivi; Mimi ni wa kwanza, na mimi ni wa mwisho; zaidi yangu mimi hapana Mungu. 7 Naye ni nani kama mimi atakayeita, na kuyahubiri haya, na kunitengenezea, tangu nilipowaweka watu wa kale? Na mambo yanayokuja na yatakayotokea, wayatangaze. 8 Msiogope wala msifanye hofu; je! Sikukuhubiri haya zamani na kuyaonyesha? Na ninyi ni mashahidi wangu. Je! Yuko Mungu zaidi yangu mimi? Hakika hapana Mwamba; mimi sijui mwingine. 9 Wachongao sanamu, wote ni ubatili; wala mambo yao yawapendezayo hayatafaa kitu; wala mashahidi wao wenyewe hawaoni, wala hawajui; ili watahayarike. 10 Ni nani aliyejichongea mungu mmoja, au aliyesubu sanamu isiyofaa kitu? 11 Tazama, wenziwe wote watatahayari; na mafundi, hao ni wanadamu; na wakusanyike pamoja, wakasimame; wataogopa na kutahayari pamoja. 12 Mfua chuma hufanza shoka, hufanya kazi kwa makaa, huitengeneza sanamu kwa nyundo, huifanyiza kwa nguvu za mkono wake; naam, huona njaa, nguvu zake zikampungukia; asipokunywa maji huzimia. 13 Seremala hunyosha uzi; huiandika kwa kalamu ya mate; huitengeneza kwa randa, huiandika kwa bikari, huifanza kwa mfano wa mwanadamu, sawasawa na uzuri wa mwanadamu, ili ikae nyumbani. 14 Yeye hujikatia mierezi, hutwaa mtiriza, na mwaloni, hujichagulia mti mmoja katika miti ya msituni; hupanda mvinje, mvua ikausitawisha. 15 Kisha utamfaa mwanadamu kwa kuni; hutwaa kipande, akaota moto; naam, huuwasha moto, akaoka mkate; naam, huufanya mungu, akauabudu; huifanya sanamu ya kuchonga, akaisujudia. 16 Sehemu moja huiteketeza; kwa sehemu nyingine hula nyama; huoka chakula kiokwacho, akashiba; naam, huota moto, akasema, Aha, nimeota moto, nimeona moto; 17 na kwa sehemu iliyobakia hufanya mungu, yaani, sanamu yake ya kuchonga; husujudu mbele yake akaiabudu, akaiomba, akasema, Uniokoe; maana wewe u mungu wangu. 18 Hawajui wala hawafikiri; maana amewafumba macho, wasione, na mioyo yao, wasiweze kufahamu. 19 Wala hapana atiaye moyoni, wala hapana maarifa, wala fahamu kusema, Nimeteketeza sehemu motoni, naam, pia nimeoka mkate juu ya makaa yake; nimeoka nyama nikaila; nami, je! Kilichobaki nikifanye kuwa chukizo? Je! Nisujudie shina la mti? 20 Hula majivu; moyo uliodanganyika umempotosha, asiweze kuiokoa nafsi yake, wala kusema, Je! Sio uongo mkononi mwangu? 21 Kumbuka haya, Ee Yakobo; nawe Israeli, maana wewe u mtumishi wangu; nimekuumba; u mtumishi wangu; Ee Israeli, hutasahauliwa na mimi. 22 Nimeyafuta makosa yako kama wingu zito, na dhambi zako kama wingu; unirudie; maana nimekukomboa. 23 Imbeni, enyi mbingu, maana Bwana ametenda hayo; Pigeni kelele, enyi mabonde ya nchi; Pazeni nyimbo, enyi milima; Nawe, msitu, na kila mti ndani yake. Maana Bwana amemkomboa Yakobo, Naye atajitukuza katika Israeli. 24 Bwana, mkombozi wako, yeye aliyekuumba tumboni, asema hivi; Mimi ni Bwana, nifanyaye vitu vyote; nizitandaye mbingu peke yangu; niienezaye nchi; ni nani aliye pamoja nami? 25 Nizitanguaye ishara za waongo, na kuwatia waganga wazimu; niwarudishaye nyuma wenye hekima, na kuyageuza maarifa yao kuwa ujinga; 26 nilithibitishaye neno la mtumishi wangu, na kuyafikiliza mashauri ya wajumbe wangu; niuambiaye Yerusalemu, Utakaliwa na watu, nayo miji ya Yuda, Itajengwa, nami nitapainua mahali pake palipobomoka; 27 niviambiaye vilindi, Kauka, nami nitaikausha mito yako; 28 nimwambiaye Koreshi, Mchungaji wangu, naye atayatenda mapenzi yangu; hata ataunena Yerusalemu, Utajengwa; na hilo hekalu, Msingi wako utawekwa.

Isaya 45

1 Haya ndiyo Bwana amwambiayo Koreshi, masihi wake,ambaye nimemshika mkono wake wa kuume,ili kutiisha mataifa mbele yake,name nitalegeza viuno vya wafalme;ili kufungua milango mbele yake,hata malango hayatafungwa. 2 Nitakwenda mbele yako, na kupasawazisha mahali palipoparuza; nitavunja vipande vipande milango ya shaba, na kukata-kata mapingo ya chuma; 3 nami nitakupa hazina za gizani, na mali zilizofichwa za mahali pa siri, upate kujua ya kuwa mimi ni Bwana, nikuitaye kwa jina lako, naam, Mungu wa Israeli. 4 Kwa ajili ya Yakobo, mtumishi wangu, na Israeli, mteule wangu, nimekuita kwa jina lako; nimekupa jina la sifa; ijapokuwa hukunijua. 5 Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine; zaidi yangu mimi hapana Mungu; nitakufunga mshipi ijapokuwa hukunijua; 6 ili wapate kujua toka maawio ya jua, na toka magharibi, ya kuwa hapana mwingine zaidi ya mimi; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine. 7 Mimi naiumba nuru, na kulihuluku giza; mimi nafanya suluhu, na kuhuluku ubaya; Mimi ni Bwana, niyatendaye hayo yote. 8 Dondokeni, enyi mbingu, toka juu, Mawingu na yamwage haki; Nchi na ifunuke, ili kutoa wokovu, Nayo itoe haki ikamee pamoja; Mimi, Bwana, nimeiumba. 9 Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini? Au kazi yako, Hana mikono? 10 Ole wake amwambiaye baba yake, Wazaa nini? Au mwanamke, Una utungu wa nini? 11 Bwana, Mtakatifu wa Israeli, na Muumba wake, asema hivi; Niulize habari za mambo yatakayokuja; mambo ya wana wangu, na habari ya kazi ya mikono yangu; haya! Niagizeni. 12 Mimi nimeiumba dunia, nimemhuluku mwanadamu juu yake; Mimi, naam, mikono yangu mimi, imezitanda mbingu, na jeshi lake lote nimeliamuru. 13 Mimi nimemwinua katika haki, nami nitazinyosha njia zake zote; ataujenga mji wangu, naye atawaacha huru watu wangu waliohamishwa, si kwa kulipwa fedha, wala kwa kupewa zawadi, asema Bwana wa majeshi. 14 Bwana asema hivi, Kazi ya Misri, na bidhaa ya Kushi, na Waseba, watu walio warefu, watakujilia, nao watakuwa wako; watakufuata; watakuja katika minyororo; wataanguka chini mbele yako, watakuomba, wakisema, Hakika Mungu yu ndani yako; wala hapana mwingine, hapana Mungu tena. 15 Hakika wewe u Mungu ujifichaye nafsi yako, Ee Mungu wa Israeli, Mwokozi. 16 Watatahayarika, naam, watafadhaika, wote pia; wale wafanyao sanamu wataingia fadhaa pamoja. 17 Bali Israeli wataokolewa na Bwana kwa wokovu wa milele; ninyi hamtatahayarika, wala kufadhaika, milele na milele. 18 Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine. 19 Sikusema kwa siri, katika mahali pa nchi ya giza; sikuwaambia wazao wa Yakobo; Nitafuteni bure; Mimi, Bwana, nasema haki; nanena mambo ya adili. 20 Jikusanyeni mje; na kukaribia pamoja, ninyi wa mataifa mliookoka; hawana maarifa wale wachukuao mti wa sanamu yao ya kuchonga; wamwombao mungu asiyeweza kuokoa. 21 Hubirini, toeni habari; naam, na wafanye mashauri pamoja; ni nani aliyeonyesha haya tangu zamani za kale? Ni nani aliyeyahubiri hapo zamani? Si mimi, Bwana? Wala hapana Mungu zaidi ya mimi; Mungu mwenye haki, mwokozi; hapana mwingine zaidi ya mimi. 22 Niangalieni mimi, mkaokolewe, enyi ncha zote za dunia; maana mimi ni Mungu; hapana mwingine. 23 Kwa nafsi yangu nimeapa, neno hili limetoka kinywani mwangu katika haki, wala halitarudi, ya kwamba mbele zangu kila goti litapigwa, kila ulimi utaapa. 24 Mmoja ataniambia, Kwa Bwana, peke yake, iko haki na nguvu; naam, watu watamwendea yeye, na wote waliomkasirikia watatahayarika. 25 Katika Bwana wazao wote wa Israeli watapewa haki, na kutukuka.

Isaya 46

1 Beli anaanguka chini, Nebo anainama; sanamu zao ziko juu ya wanyama, na juu ya ng'ombe; vitu vile mlivyokuwa mkivichukua huku na huku vimekuwa mzigo, mzigo wa kumlemea mnyama aliyechoka. 2 Wanajiinamisha, wanainama pamoja; hawakuweza kuutua mzigo, bali wao wenyewe wamekwenda kufungwa. 3 Nisikilizeni, enyi wa nyumba ya Yakobo, ninyi mlio mabaki ya nyumba ya Israeli, mliochukuliwa nami tangu tumboni, mlioinuliwa tangu mimbani; 4 na hata uzee wenu mimi ndiye, na hata wakati wenu wa mvi nitawachukueni; nimefanya, nami nitachukua; naam, nitachukua na kuokoa. 5 Mtanifananisha na nani, na kunisawazisha naye, na kunilinganisha naye, ili tuwe sawasawa? 6 Watu wamwagao dhahabu kutoka mfukoni, na kupima fedha katika mizani, huajiri mfua dhahabu, akaifanya mungu; huanguka, naam, huabudu. 7 Humchukua begani, humchukua, wakamsimamisha mahali pake, akasimama; hataondoka katika mahali pake, naam, mmoja atamwita, lakini hawezi kujibu, wala kumwokoa na taabu yake. 8 Kumbukeni haya, mkajionyeshe kuwa waume; jifahamisheni haya, ninyi mkosao; 9 kumbukeni mambo ya zamani za kale; maana mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; 10 nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote. 11 Nikiita ndege mkali kutoka mashariki, mtu wa shauri langu toka nchi iliyo mbali; naam, nimenena, nami nitatekeleza; nimekusudia, nami nitafanya. 12 Nisikilizeni, ninyi mlio na moyo mshupavu, mlio mbali na haki; 13 Mimi ninaleta karibu haki yangu, haitakuwa mbali, na wokovu wangu hautakawia; nami nitaweka wokovu katika Sayuni kwa ajili ya Israeli, utukufu wangu.

Isaya 47

1 Haya, shuka, keti mavumbini, Ewe bikira, binti Babeli; Keti chini pasipo kiti cha enzi, Ewe binti wa Wakaldayo; Maana hutaitwa tena mwororo, mpenda anasa. 2 Twaa mawe ya kusagia, usage unga; Vua utaji wako, ondoa mavazi yako, Funua mguu wako, pita katika mito ya maji. 3 Uchi wako utafunuliwa, Naam, aibu yako itaonekana. Nitalipa kisasi; simkubali mtu ye yote. 4 Mkombozi wetu, Bwana wa majeshi ndilo jina lake, Mtakatifu wa Israeli. 5 Kaa kimya, ingia gizani, Ee binti wa Wakaldayo; Maana hutaitwa tena Malkia wa falme. 6 Nalikuwa nimekasirika na watu wangu, naliutia unajisi urithi wangu, nikawatia mkononi mwako; wewe hukuwatendea rehema; uliwatia wazee nira yako, nayo nzito sana. 7 Ukasema, Mimi nitakuwa bibi milele; hata hukuyatia hayo moyoni mwako, wala hukukumbuka mwisho wa mambo hayo. 8 Sasa, basi, sikia haya, wewe upendaye anasa, ukaaye na kujiona salama, wewe usemaye moyoni mwako, Mimi ndiye, wala hapana mwingine zaidi yangu mimi; sitaketi mfano wa mjane, wala sitajua kufiwa na watoto; 9 lakini mambo haya mawili yatakupata katika dakika moja siku moja, kufiwa na watoto, na ujane; yatakupata kiasi kitimilifu, uchawi wako ujapokuwa mwingi, na uganga wako mwingi mno. 10 Maana umeutumainia ubaya wako; umesema, Hapana anionaye; hekima yako, na maarifa yako yamekupotosha, nawe umesema moyoni mwako, Mimi ndiye, wala hapana mwingine zaidi yangu mimi. 11 Kwa sababu hiyo ubaya utakupata; wala hutajua kutopoa kwake; na msiba utakuangukia; hutaweza kuuondoa; na ukiwa utakupata kwa ghafula, usioujua. 12 Simama sasa na uganga wako, na wingi wa uchawi wako, uliojitaabisha nao tangu ujana wako; labda utaweza kupata faida, labda utaweza kushinda. 13 Umechoka kwa wingi wa mashauri yako; basi, na wasimame hao wajuao falaki, wazitazamao nyota, watabirio kila mwezi mambo ya mwezi huo, wakakuokoe na mambo yatakayokupata. 14 Tazama, watakuwa kama mabua makavu; moto utawateketeza; hawatajiokoa na nguvu za mwali wa moto; hautakuwa kaa la kukota moto, wala moto wa kukaa karibu nao. 15 Ndivyo yatakavyokuwa mambo hayo uliyojitaabisha nayo; wale waliofanya biashara nawe tangu ujana wako watatanga-tanga mbali nawe, kila mtu akienda zake; hapatakuwa na mtu wa kukuokoa.

Isaya 48

1 Sikieni haya, enyi watu wa nyumba ya Yakobo, mnaoitwa kwa jina la Israeli, mliotoka katika maji ya Yuda; mnaoapa kwa jina la Bwana, na kumtaja Mungu wa Israeli, lakini si kwa kweli, wala si kwa haki. 2 Maana hujiita wenyeji wa mji mtakatifu, hujitegemeza juu ya Mungu wa Israeli; Bwana wa majeshi ni jina lake. 3 Mimi nimehubiri mambo ya kale tangu zamani; naam, yalitoka katika kinywa changu, nikayadhihirisha; naliyatenda kwa ghafula, yakatokea. 4 Kwa sababu nalijua ya kuwa wewe u mkaidi, na shingo yako ni shingo ya chuma, na kipaji cha uso wako ni shaba; 5 basi nimekuonyesha tangu zamani; kabla hayajatukia nalikuonyesha; usije ukasema, Sanamu yangu imetenda haya; sanamu yangu ya kuchonga, na sanamu yangu ya kuyeyusha, imeyaamuru. 6 Umesikia haya; tazama haya yote; nanyi, je! Hamtayahubiri? Nimekuonyesha mambo mapya tangu wakati huu, naam, mambo yaliyofichwa, usiyoyajua. 7 Yameumbwa sasa, wala si tokea zamani; na kabla ya siku hii ya leo hukusikia habari yake; usije ukasema, Tazama, naliyajua. 8 Naam, hukusikia; naam, hukujua; naam, tokea zamani sikio lako halikuzibuka; maana nalijua ya kuwa wewe watenda kwa hila nyingi, nawe umeitwa mkosaji tangu kuzaliwa kwako; 9 kwa ajili ya jina langu nitaahirisha hasira yangu, na kwa ajili yako nitajizuia, ili nisifiwe, wala nisikukatilie mbali. 10 Tazama, nimekusafisha, lakini si kama fedha; nimekuchagua katika tanuru ya mateso. 11 Kwa ajili ya nafsi yangu, kwa ajili ya nafsi yangu, nitatenda haya; je! Litiwe unajisi jina langu? Wala sitampa mwingine utukufu wangu. 12 Nisikilize mimi, Ee Yakobo; na Israeli, niliyekuita; mimi ndiye. Mimi ni wa kwanza, na mimi ni wa mwisho pia. 13 Naam, mkono wangu umeuweka msingi wa dunia, na mkono wangu wa kuume umezitanda mbingu; niziitapo husimama pamoja. 14 Kusanyikeni, ninyi nyote, mkasikie; ni nani miongoni mwao aliyehubiri haya? Bwana amempenda; atatimiza mapenzi yake juu ya Babeli, na mkono wake utakuwa juu ya Wakaldayo. 15 Mimi, naam, mimi, nimenena; naam, nimemwita; nimemleta, naye ataifanikisha njia yake. 16 Nikaribieni, sikieni haya; tokea mwanzo sikunena kwa siri; tangu yalipokuwapo, mimi nipo; na sasa Bwana MUNGU amenituma, na roho yake. 17 Bwana, mkombozi wako, mtakatifu wa Israeli, asema hivi; Mimi ni Bwana, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. 18 Laiti ungalisikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari; 19 Tena wazao wako wangalikuwa kama mchanga, na hao waliotoka katika tumbo lako kama chembe zake; jina lake lisingalikatika, wala kufutwa mbele zangu. 20 Haya, tokeni katika Babeli, Kimbieni kutoka kwa Wakaldayo; Hubirini kwa sauti ya kuimba, tangazeni haya, Yatamkeni mpaka mwisho wa dunia, semeni, Bwana amemkomboa mtumishi wake, Yakobo. 21 Wala hawakuona kiu alipowaongoza jangwani; Alitoa maji katika mwamba kwa ajili yao; Pia akaupasua mwamba, maji yakatoka kwa nguvu. 22 Hapana amani kwa wabaya, asema Bwana.

Isaya 49

1 Nisikilizeni, enyi visiwa; tegeni masikio yenu, enyi kabila za watu mlio mbali sana; Bwana ameniita tangu tumboni; toka tumbo la mama yangu amenitaja jina langu. 2 Naye anifanya kinywa changu kuwa kama upanga mkali; katika kivuli cha mkono wake amenisitiri; naye amenifanya kuwa mshale uliosuguliwa; katika podo lake amenificha; 3 akaniambia; Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa. 4 Lakini nikasema, Nimejitaabisha bure, nimetumia nguvu zangu bure bila faida; lakini hakika hukumu yangu ina Bwana, na thawabu yangu ina Mungu wangu. 5 Na sasa Bwana asema hivi, yeye aliyeniumba tangu tumboni niwe mtumishi wake, ili nimletee Yakobo tena, na Israeli wakusanyike mbele zake tena; (maana mimi nimepata heshima mbele ya macho ya Bwana, na Mungu wangu amekuwa nguvu zangu); 6 naam, asema hivi, Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuziinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifadhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia. 7 Bwana, mkombozi wa Israeli, Mtakatifu wake, amwambia hivi yeye anayedharauliwa na wanadamu; yeye anayechukiwa na taifa hili; yeye aliye mtumishi wao watawalao; Wafalme wataona, watasimama; wakuu nao watasujudu; kwa sababu ya Bwana aliye mwaminifu, Mtakatifu wa Israeli aliyekuchagua 8 Bwana asema hivi, Wakati uliokubalika nimekujibu, na siku ya wokovu nimekusaidia; nami nitakuhifadhi, nitakutoa uwe agano la watu hawa, ili kuiinua nchi hii, na kuwarithisha urithi uliokuwa ukiwa; 9 kuwaambia waliofungwa, Haya, tokeni; na hao walio katika giza, Jionyesheni. Watajilisha katika njia, na juu ya majabali watapata malisho. 10 Hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza. 11 Nami nitafanya milima yangu yote kuwa njia, na njia kuu zangu zitatukuzwa zote. 12 Tazama, hawa watakuja kutoka mbali; na tazama, hawa kutoka kaskazini, na kutoka magharibi, na hawa kutoka nchi ya Sinimu. 13 Imbeni, enyi mbingu; ufurahi, Ee nchi; Pazeni sauti ya kuimba, enyi milima; Kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, Naye atawahurumia watu wake walioteswa. 14 Bali Sayuni alisema, YEHOVA ameniacha, Bwana amenisahau. 15 Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe. 16 Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima. 17 Watoto wako wafanya haraka, hao wakuharibuo, nao waliokufanya ukiwa, watatoka kwako. 18 Inua macho yako, ukatazame pande zote; hao wote wanajikusanya na kukujia. Kama niishivyo, asema Bwana, hakika utajivika na hao wote, kama kwa uzuri, nawe utajifungia hao, kama bibi arusi. 19 Maana katika habari za mahali pako palipokuwa ukiwa, pasipokaliwa na watu, na nchi yako iliyoharibika hakika sasa utakuwa mwembamba usiwatoshe wenyeji wako, nao waliokumeza watakuwa mbali. 20 Watoto ulionyang'anywa watasema masikioni mwako, Mahali hapa ni pembamba, hapanitoshi; nipe nafasi nipate kukaa. 21 Ndipo utasema moyoni mwako, Ni nani aliyenizalia watoto hawa, na mimi nimefiwa na watoto wangu, nami ni peke yangu, nimehamishwa, ninatanga-tanga huko na huku? Tena ni nani aliyewalea hawa? Tazama, naliachwa peke yangu; hawa je! Walikuwa wapi? 22 Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, nitawainulia mataifa mkono wangu, na kuwatwekea kabila za watu bendera yangu; nao wataleta wana wako vifuani mwao, na binti zako watachukuliwa mabegani mwao. 23 Na wafalme watakuwa baba zako za kulea, na malkia zao mama zako za kulea; watainama mbele yako kifudifudi, na kuramba mavumbi ya miguu yako; nawe utajua ya kuwa mimi ni Bwana, tena waningojeao hawatatahayarika. 24 Je! Aliye hodari aweza kunyang'anywa mateka yake, au jeshi lao waliofungwa halali wataokoka? 25 Naam, Bwana asema hivi, Hata jeshi la wafungwa wake aliye hodari watapokonywa mikononi mwake, na mateka yake aliye jabari wataokoka; kwa maana nitateta na yeye atetaye nawe, nami nitawaletea wana wako wokovu. 26 Na hao wanaokuonea nitawalisha nyama yao wenyewe, nao watalewa kwa kuinywa damu yao wenyewe, kama kwa mvinyo mpya; na wote wenye mwili watajua ya kuwa mimi, Bwana, ni mwokozi wako, na Mkombozi wako ni Mwenye enzi wa Yakobo.

Isaya 50

1 Bwana asema hivi, Iko wapi hati ya talaka ya mama yenu, ambayo kwa hiyo naliachana naye? Au nimewauza ninyi kwa nani katika watu wanaoniwia? Ninyi mliuzwa kwa sababu ya maovu yenu; tena mama yenu ameachwa kwa sababu ya makosa yenu. 2 Basi, nilipokuja, mbona hapakuwa na mtu? Nilipoita, mbona hapakuwa na mtu aliyenijibu? Je! Mkono wangu ni mfupi, hata nisiweze kukomboa? Au je! Mimi sina nguvu za kuponya? Tazama, kwa kukemea kwangu naikausha bahari, mito ya maji naifanya kuwa jangwa; samaki wao wanuka kwa sababu hapana maji, nao wafa kwa kiu. 3 Mimi nazivika mbingu weusi, nami nafanya nguo ya magunia kuwa kifuniko chao. 4 Bwana MUNGU amenipa ulimi wa hao wafundishwao, nipate kujua jinsi ya kumtegemeza kwa maneno yeye aliyechoka, huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao. 5 Bwana MUNGU amenizibua sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala sikurudi nyuma. 6 Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang'oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate. 7 Maana Bwana MUNGU atanisaidia; kwa sababu hiyo sikutahayari, kwa sababu hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume, nami najua ya kuwa sitaona haya. 8 Yeye anipatiaye haki yangu yu karibu; ni nani atakayeshindana nami? Na tusimame pamoja; ni nani aliye hasimu yangu? Na anikaribie basi. 9 Tazama, Bwana MUNGU atanisaidia; ni nani atakayenihukumu kuwa mkosa? Tazama hao wote watachakaa kama vazi; nondo atawala. 10 Ni nani miongoni mwenu amchaye Bwana, aitiiye sauti ya mtumishi wake? Yeye aendaye katika giza, wala hana nuru, naye alitumainia jina la Bwana, na kumtegemea Mungu wake. 11 Tazama, ninyi nyote mwashao moto, mjifungiao hiyo mienge; endeni ninyi katika mwali wa moto wenu, na katikati ya mienge mliyoiwasha. Mtayapata haya kwa mkono wangu; mtalala kwa huzuni.

Isaya 51

1 Nisikilizeni, ninyi mnaoifuatia haki; ninyi mnaomtafuta Bwana; uangalieni mwamba ule ambao mlitolewa kwa kuchongwa, na tundu la shimo ambalo mlitolewa kwa kuchimbuliwa. 2 Mwangalieni Ibrahimu, baba yenu, na Sara, aliyewazaa; kwa maana alipokuwa mmoja tu nalimwita, nikambariki, nikamfanya kuwa wengi. 3 Maana Bwana ameufariji Sayuni; amepafariji mahali pake palipokuwa ukiwa; amefanya jangwa lake kuwa kama bustani ya Edeni, na nyika yake kama bustani ya Bwana; furaha na kicheko zitaonekana ndani yake, kushukuru, na sauti ya kuimba. 4 Nisikilizeni mimi, enyi watu wangu; nisikieni, taifa langu; maana sheria itatoka kwangu, nami nitaistarehesha hukumu yangu iwe nuru ya mataifa. 5 Haki yangu i karibu, wokovu wangu umekuwa wazi, na mikono yangu itawahukumu kabila za watu; visiwa vitaningoja, navyo vitautumainia mkono wangu. 6 Inueni macho yenu mbinguni, mkaitazame nchi chini; maana mbingu zitatoweka kama moshi, na nchi itachakaa kama vazi, nao wakaao ndani yake watakufa kadhalika; bali wokovu wangu utakuwa wa milele, na haki yangu haitatanguka. 7 Nisikilizeni, ninyi mjuao haki, watu ambao mioyoni mwenu mna sheria yangu; msiogope matukano ya watu, wala msifadhaike kwa sababu ya dhihaka zao. 8 Maana nondo itawala kama vazi, na funza atawala kama sufu; bali haki yangu itakuwa ya milele, na wokovu wangu hata vizazi vyote. 9 Amka, amka, jivike nguvu, Ee mkono wa Bwana; Amka kama katika siku zile za kale, Katika vizazi vile vya zamani. 10 Si wewe uliyemkata-kata Rahabu? Uliyemchoma yule joka? Si wewe uliyeikausha bahari, Na maji ya vilindi vikuu; Uliyevifanya vilindi kuwa njia, Ili wapite watu waliokombolewa? 11 Nao waliokombolewa na Bwana watarejea, Watafika Sayuni, wakiimba; Furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao; Watapata shangwe na furaha; Huzuni na kuugua zitakimbia. 12 Mimi, naam, mimi, ndimi niwafarijiye; wewe u nani hata ukamwogopa mtu atakayekufa, na mwanadamu atakayefanywa kuwa kama majani? 13 Ukamsahau Bwana, Muumba wako, yeye aliyezitanda mbingu, na kuiweka misingi ya dunia; nawe unaogopa daima mchana kutwa kwa sababu ya ghadhabu yake yeye aoneaye, hapo afanyapo tayari kuharibu; nayo i wapi ghadhabu yake aoneaye? 14 Yeye aliyehamishwa na kufungwa atafunguliwa kwa haraka; wala hatakufa na kushuka shimoni, wala chakula chake hakitapunguka. 15 Maana mimi ni Bwana, Mungu wako, niichafuaye bahari, mawimbi yake yakavuma. 16 Bwana wa majeshi ndilo jina lake. Nami nimetia maneno yangu kinywani mwako, nami nimekusitiri katika kivuli cha mkono wangu, ili nizipande mbingu, na kuiweka misingi ya dunia, na kuuambia Sayuni, Ninyi ni watu wangu. 17 Amka, amka, simama, Ee Yerusalemu, Wewe uliyenywea, mkononi mwa Bwana, Kikombe cha hasira yake; Bakuli la kikombe cha kulevya-levya Umelinywea na kulimaliza. 18 Hapana hata mmoja wa kumwongoza Miongoni mwa wana wote aliowazaa, Wala hapana hata mmoja wa kumshika mkono Miongoni mwa wana wote aliowalea. 19 Mambo haya mawili yamekupata; Ni nani awezaye kukusikitikia? Ukiwa na uharibifu, na njaa na upanga; Niwezeje kukutuliza? 20 Wana wako wamezimia, Wamelala penye pembe za njia kuu zote Kama kulungu wavuni; Wamejaa hasira ya Bwana, Lawama ya Mungu wako. 21 Basi, kwa sababu ya hayo, ulisikilize neno hili, ewe uliyeteswa, na kulewa, lakini si kwa mvinyo; 22 Bwana, Bwana wako na Mungu wako, awateteaye watu wake, asema hivi, Tazama, nimeondoa mkononi mwako kikombe cha kulevya-levya, hilo bakuli la kikombe cha hasira yangu; hutakinywea tena; 23 nami nitakitia mikononi mwao wakutesao; waliokuambia nafsi yako, Inama, tupate kupita; nawe uliufanya mgongo wako kuwa kama nchi, na kama njia, kwa hao wapitao juu yake.

Isaya 52

1 Amka, amka, jivike nguvu zako, Ee Sayuni; Jivike mavazi yako mazuri, Ee Yerusalemu, mji mtakatifu; Kwa maana tokea sasa hataingia ndani yako Asiyetahiriwa, wala aliye najisi. 2 Jikung'ute mavumbi; uondoke, Uketi, Ee Yerusalemu; Jifungulie vifungo vya shingo yako, Ee binti Sayuni uliyefungwa. 3 Maana Bwana asema hivi, Mliuzwa bure; nanyi mtakombolewa bila fedha. 4 Maana Bwana MUNGU asema hivi, Watu wangu hapo kwanza walishuka Misri ili wakae huko hali ya ugeni; na Mwashuri akawaonea bila sababu. 5 Basi sasa, nafanya nini hapa, asema Bwana, ikiwa watu wangu wamechukuliwa bure? Hao wanaowatawala wanapiga yowe, asema Bwana, na jina langu linatukanwa daima mchana kutwa. 6 Kwa hiyo watu wangu watalijua jina langu kwa hiyo watajua siku ile ya kuwa mimi ndimi ninenaye; tazama ni mimi. 7 Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima Miguu yake aletaye habari njema, Yeye aitangazaye amani, Aletaye habari njema ya mambo mema, Yeye autangazaye wokovu, Auambiaye Sayuni, Mungu wako anamiliki! 8 Sauti ya walinzi wako! Wanapaza sauti zao, wanaimba pamoja; Maana wataona jicho kwa jicho, Jinsi Bwana arejeavyo Sayuni. 9 Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja, Enyi mahali pa Yerusalemu palipokuwa ukiwa; Kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, Ameukomboa Yerusalemu. 10 Bwana ameweka wazi mkono wake mtakatifu Machoni pa mataifa yote; Na ncha zote za dunia Zitauona wokovu wa Mungu wetu. 11 Nendeni zenu, nendeni zenu, tokeni huko, msiguse kitu kichafu; tokeni kati yake; iweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya Bwana. 12 Maana hamtatoka kwa haraka, wala hamtakwenda kwa kukimbia, kwa sababu Bwana atawatangulia; na Mungu wa Israeli atawafuata nyuma; awalinde. 13 Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa busara, atatukuzwa, na kuinuliwa juu, naye atakuwa juu sana. 14 Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu), 15 ndivyo atakavyowasitusha mataifa mengi; wafalme watamfumbia vinywa vyao; maana mambo wasiyoambiwa watayaona; na mambo wasiyoyasikia watayafahamu.

Isaya 53

1 Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani? 2 Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. 3 Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. 4 Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. 5 Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. 6 Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. 7 Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. 8 Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. 9 Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake. 10 Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; 11 Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao. 12 Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.

Isaya 54

1 Imba, wewe uliye tasa, wewe usiyezaa; paza sauti yako kwa kuimba, piga kelele, wewe usiyekuwa na utungu; maana watoto wake aliyeachwa ni wengi kuliko watoto wake yeye aliyeolewa, asema Bwana. 2 Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako; usiwakataze; ongeza urefu wa kamba zako; vikaze vigingi vya hema yako. 3 Kwa maana utaenea upande wa kuume na upande wa kushoto; na wazao wako watawamiliki mataifa; wataifanya miji iliyokuwa ukiwa kukaliwa na watu. 4 Usiogope; maana hutatahayarika; wala usifadhaike; maana hutaaibishwa; kwa kuwa utaisahau aibu ya ujana wako, pia mashutumu ya ujane wako hutayakumbuka tena. 5 Kwa sababu Muumba wako ni mume wako; Bwana wa majeshi ndilo jina lake; na Mtakatifu wa Israeli ndiye Mkombozi wako; Yeye ataitwa Mungu wa dunia yote. 6 Maana Bwana amekuita kama mke aliyeachwa na kuhuzunishwa rohoni, kama mke wakati wa ujana, atupwapo, asema Mungu wako. 7 Kwa kitambo kidogo nimekuacha; lakini kwa rehema nyingi nitakukusanya. 8 Kwa ghadhabu ifurikayo nalikuficha uso wangu dakika moja; lakini kwa fadhili za milele nitakurehemu, asema Bwana, Mkombozi wako. 9 Kwa maana jambo hili limekuwa kama maji ya Nuhu kwangu; maana kama nilivyoapa ya kwamba maji ya Nuhu hayatapita juu ya dunia tena, kadhalika nimeapa ya kwamba sitakuonea hasira, wala kukukemea. 10 Maana milima itaondoka, na vilima vitaondolewa; bali wema wangu hautaondoka kwako, wala agano langu la amani halitaondolewa; asema Bwana akurehemuye. 11 Ewe uliyeteswa, uliyerushwa na tufani, usiyetulizwa, tazama, nitaweka mawe yako kwa rangi nzuri, nitaweka misingi yako kwa yakuti samawi. 12 Nami nitaifanya minara yako ya akiki nyekundu, na malango yako ya almasi, na mipaka yako yote ya mawe yapendezayo. 13 Na watoto wako wote watafundishwa na Bwana; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi. 14 Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia. 15 Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako. 16 Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. 17 Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.

Isaya 55

1 Haya, kila aonaye kiu, njoni majini, Naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; Naam, njoni, nunueni divai na maziwa, Bila fedha na bila thamani. 2 Kwani kutoa fedha kwa ajili ya kitu ambacho si chakula? Na mapato yenu kwa kitu kisichoshibisha? Nisikilizeni kwa bidii, mle kilicho chema, Na kujifurahisha nafsi zenu kwa unono. 3 Tegeni masikio yenu, na kunijia; Sikieni, na nafsi zenu zitaishi; Nami nitafanya nanyi agano la milele, Naam, rehema za Daudi zilizo imara. 4 Angalieni, nimemweka kuwa shahidi kwa kabila za watu; kuwa kiongozi na jemadari kwa kabila za watu. 5 Tazama, utaita taifa usilolijua, na taifa lisilokujua wewe litakukimbilia, kwa sababu ya Bwana, Mungu wako, na kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli; maana amekutukuza. 6 Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu; 7 Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa. 8 Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. 9 Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu. 10 Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; 11 ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma. 12 Maana mtatoka kwa furaha, Mtaongozwa kwa amani; Mbele yenu milima na vilima vitatoa nyimbo; Na miti yote ya kondeni itapiga makofi. 13 Badala ya michongoma utamea msunobari, Na badala ya mibigili, mhadesi; Jambo hili litakuwa la kumpatia Bwana jina, Litakuwa ishara ya milele isiyokatiliwa mbali.

Isaya 56

1 Bwana asema hivi, Shikeni hukumu, mkatende haki; kwa maana wokovu wangu u karibu kuja, na haki yangu kufunuliwa. 2 Heri afanyaye haya, na mwanadamu ayashikaye sana; azishikaye sabato asizivunje, auzuiaye mkono wake usifanye uovu wo wote. 3 Wala mgeni, aambatanaye na Bwana, asiseme hivi, Hakika yake Bwana atanitenga na watu wake; wala towashi asiseme, Mimi ni mti mkavu. 4 Kwa maana Bwana awaambia hivi matowashi, wanaozishika sabato zangu, na kuyachagua mambo yanipendezayo, na kulishika sana agano langu; 5 Nitawapa hawa nyumbani mwangu, na ndani ya kuta zangu, kumbukumbu na jina, lililo jema kuliko kuwa na wana na binti; nitawapa jina lidumulo milele, lisilokatiliwa mbali. 6 Na wageni, walioandamana na Bwana ili wamhudumu, na kulipenda jina la Bwana, kuwa watumishi wake; kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika sana agano langu; 7 Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; makafara yao na dhabihu zao zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote. 8 Bwana MUNGU, akusanyaye waliofukuzwa katika Israeli asema, Pamoja na hayo nitamkusanyia na wengine, zaidi ya hao walio wake waliokusanywa. 9 Enyi hayawani wote wa nyikani, njoni, Mle, enyi hayawani wote wa mwituni. 10 Walinzi wake ni vipofu, wote pia hawana maarifa; wote ni mbwa walio bubu, hawawezi kulia; huota ndoto, hulala, hupenda usingizi. 11 Naam, mbwa hao wana choyo sana, hawashibi kamwe; na hao ni wachungaji wasioweza kufahamu neno; wote pia wamegeuka upande, wazifuate njia zao wenyewe, kila mmoja kwa faida yake, toka pande zote. 12 Husema, Njoni, nitaleta divai, Na tunywe sana kileo; Na kesho itakuwa kama leo, Sikukuu kupita kiasi.

Isaya 57

1 Mwenye haki hupotea, wala hakuna atiaye hayo moyoni; na watu watauwa huondolewa, wala hakuna afikiriye ya kuwa mwenye haki ameondolewa asipatikane na mabaya. 2 Yeye huingia katika amani; wao hustarehe katika vitanda vyao, kila mtu aendaye katika unyofu wake. 3 Lakini ninyi karibuni hapa, enyi wana wa mwanamke mchawi, uzao wa mzinzi na kahaba. 4 Mnafanya dhihaka yenu juu ya nani? Mmepanua vinywa vyenu, na kutoa ndimi zenu? Je, ninyi si wana wa uasi, uzao wa uongo; 5 ninyi mnaowasha tamaa zenu kati ya mialoni, chini ya kila mti wenye majani mabichi; ninyi mnaoua watoto mabondeni, chini ya mianya ya majabali? 6 Sehemu yako i katika makokoto ya bonde; hayo ndiyo kura yako; umeyamwagia hayo sadaka ya kinywaji, umeyatolea sadaka ya unga; je! Niwe radhi na mambo hayo? 7 Umeweka kitanda chako juu ya mlima mrefu ulioinuka sana; ukaenda huko ili kutoa dhabihu. 8 Na nyuma ya milango na miimo umeweka kumbukumbu lako; kwa maana umejifunua nafsi yako kwa ajili ya mwingine, si kwa ajili yangu, ukakwea juu; umekipanua kitanda chako, nawe umefanya maagano na hao; ulikipenda kitanda chao hapo ulipokiona. 9 Ulimwendea mfalme na mafuta ya marhamu, ukaongeza manukato yako, ukawatuma wajumbe wako waende mbali, ukajidhili sana hata kuzimu. 10 Ulikuwa umechoka kwa ajili ya urefu wa njia yako; lakini hukusema, Hapana matumaini; ulipata kuhuishwa nguvu zako; kwa sababu hiyo hukuugua. 11 Tena ni nani uliyemwogopa na kumhofu, hata ukasema uongo, wala hukunikumbuka mimi, wala kuweka hayo moyoni? Je! Mimi sikunyamaza tangu zamani, hata huniogopi? 12 Mimi nitatangaza haki yako, na matendo yako hayatakufaa. 13 Utakapolia, na wakuponye hao uliowakusanya; lakini upepo utawachukua; uvuvio tu utawachukulia mbali; lakini yeye anayenitumaini ataimiliki nchi, na kuurithi mlima wangu mtakatifu. 14 Naye atasema, Tutieni, tutieni, Itengenezeni njia, Kiondoeni kila kikwazacho Katika njia ya watu wangu. 15 Maana yeye aliye juu, aliyetukuka, akaaye milele; ambaye jina lake ni Mtakatifu; asema hivi; Nakaa mimi mahali palipoinuka, palipo patakatifu; tena pamoja na yeye aliye na roho iliyotubu na kunyenyekea, ili kuzifufua roho za wanyenyekevu, na kuifufua mioyo yao waliotubu. 16 Kwa kuwa sitashindana na watu siku zote, wala sitakuwa na hasira siku zote; maana roho ingezimia mbele zangu, na hizo nafsi nilizozifanya. 17 Kwa sababu ya uovu wa kutamani kwake naliona hasira, nikampiga; nalificha uso wangu, nikaona ghadhabu; naye akaendelea kwa ukaidi, kuifuata njia ya moyo wake mwenyewe. 18 Nimeziona njia zake; nami nitamponya; nitamwongoza pia, nitamrudishia faraja zake, yeye na hao wanaomlilia. 19 Mimi nayaumba matunda ya midomo; Amani, amani, kwake yeye aliye mbali, na kwake yeye aliye karibu; asema Bwana; nami nitamponya. 20 Bali wabaya wanafanana na bahari iliyochafuka; maana haiwezi kutulia, na maji yake hutoa tope na takataka. 21 Hapana amani kwa wabaya; asema Mungu wangu.

Isaya 58

1 Piga kelele, usiache, Paza sauti yako kama tarumbeta; Uwahubiri watu wangu kosa lao, Na nyumba ya Yakobo dhambi zao. 2 Walakini wanitafuta kila siku; hupenda kujua njia zangu; kama vile taifa waliotenda haki, wasioacha sheria ya Mungu wao, hutaka kwangu amri za haki; hufurahi kumkaribia Mungu. 3 Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu. 4 Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uovu. Hamfungi siku hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu. 5 Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana? 6 Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? 7 Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe? 8 Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde. 9 Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa. Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu; 10 na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri. 11 Naye Bwana atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, na kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui. 12 Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia. 13 Kama ukigeuza mguu wako usihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya Bwana yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo, wala kusema maneno yako mwenyewe; 14 ndipo utakapojifurahisha katika Bwana; nami nitakupandisha mahali pa nchi palipoinuka; nitakulisha urithi wa Yakobo baba yako; kwa maana kinywa cha Bwana kimenena hayo.

Isaya 59

1 Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; 2 lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia. 3 Kwa maana mikono yenu imetiwa unajisi kwa damu, na vidole vyenu vimetiwa unajisi kwa uovu; midomo yenu imenena uongo, ndimi zenu zimenong'ona ubaya. 4 Hapana adaiye kwa haki, wala hapana atetaye kwa kweli; hutumainia ubatili, hunena uongo; hupata mimba ya madhara, na kuzaa uovu. 5 Huangua mayai ya fira, na kusuka wavu wa buibui; yeye alaye mayai yao hufa, na hilo livunjwalo hutoka nyoka. 6 Nyavu zao hazitakuwa mavazi, wala hawatajifunika kwa kazi zao; kazi zao ni kazi za uovu, na vitendo vya udhalimu vimo mikononi mwao. 7 Miguu yao hukimbilia mabaya, nao hufanya haraka kumwaga damu isiyo na hatia; mawazo yao ni mawazo ya uovu; ukiwa na uharibifu zaonekana katika njia kuu zao. 8 Njia ya amani hawaijui; wala hapana hukumu ya haki katika miendo yao; wamejifanyizia njia zilizopotoka; kila apitaye katika njia hizo hajui amani. 9 Kwa sababu hiyo hukumu ya haki i mbali nasi, wala haki haitufikilii; twatazamia nuru, na kumbe! Latokea giza; twatazamia mwanga, lakini twaenda katika giza kuu. 10 Twapapasa-papasa kutafuta ukuta kama kipofu, naam, twapapasa kama watu wasio na macho; twajikwaa wakati wa adhuhuri, kana kwamba ni wakati wa ukungu wa alfajiri; kati yao waliowanda tumekuwa kama wafu. 11 Sisi sote twanguruma kama dubu; twaomboleza kama hua; twatazamia hukumu ya haki, lakini hapana; na wokovu, lakini u mbali nasi. 12 Maana makosa yetu yamezidi kuwa mengi mbele zako, na dhambi zetu zashuhudia juu yetu; maana makosa yetu tunayo pamoja nasi, na maovu yetu tumeyajua; 13 katika kukosa na kumkana Bwana, na katika kugeuka tusimfuate Mungu wetu, tukinena jeuri na uasi, na kukusudia maneno ya uongo na kuyatoa moyoni. 14 Na hukumu imegeuka ikaenda nyuma, na haki inasimama mbali sana; maana kweli imeanguka katika njia kuu, na unyofu hauwezi kuingia. 15 Naam, kweli imepunguka kabisa, na yeye auachaye uovu ajifanya kuwa mateka; naye Bwana akaona hayo, akachukizwa kwa kuwa hapana hukumu ya haki. 16 Akaona ya kuwa hapana mtu, akastaajabu kwa kuwa hapana mwombezi; basi, mkono wake mwenyewe ndio uliomletea wokovu; na haki yake ndiyo iliyomsaidia. 17 Akajivika haki kama deraya kifuani, na chapeo cha wokovu kichwani pake, akajivika mavazi ya kisasi yawe mavazi yake, naye alivikwa wivu kama joho. 18 Kadiri ya matendo yao, kwa kadiri iyo hiyo atawalipa, ukali kwao wampingao, malipo kwa adui zake; naye atavirudishia visiwa malipo. 19 Basi, wataliogopa jina la Bwana toka magharibi, na utukufu wake toka maawio ya jua; maana yeye atakuja kama mkondo wa mto ufurikao, uendeshwao kwa pumzi ya Bwana. 20 Na Mkombozi atakuja Sayuni, kwao waachao maasi yao katika Yakobo, asema Bwana. 21 Tena katika habari zangu, hili ndilo agano langu nao, asema Bwana; roho yangu iliyo juu yako, na maneno yangu niliyoyatia kinywani mwako, hayataondoka kinywani mwako, wala kinywani mwa wana wako, wala kinywani mwa wajukuu wako, asema Bwana, tangu leo na hata milele.

Isaya 60

1 Ondoka, uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, Na utukufu wa Bwana umekuzukia. 2 Maana, tazama, giza litaifunika dunia, Na giza kuu litazifunika kabila za watu; Bali Bwana atakuzukia wewe, Na utukufu wake utaonekana juu yako. 3 Na mataifa wataijilia nuru yako, Na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako. 4 Inua macho yako, utazame pande zote; Wote wanakusanyana; wanakujia wewe; Wana wako watakuja kutoka mbali. Na binti zako watabebwa nyongani. 5 Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, Na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; Kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, Utajiri wa mataifa utakuwasilia. 6 Wingi wa ngamia utakufunika, Ngamia vijana wa Midiani na Efa; Wote watakuja kutoka Sheba; Wataleta dhahabu na uvumba; Na kuzitangaza sifa za Bwana. 7 Makundi yote ya Kedari yatakusanyika kwako, Kondoo waume wa Nebayothi watakutumikia; Watapanda juu ya madhabahu yangu kwa kibali, Nami nitaitukuza nyumba ya utukufu wangu. 8 Ni nani hawa warukao kama wingu, Na kama njiwa waendao madirishani kwao? 9 Hakika yake visiwa vitaningojea, Na merikebu za Tarshishi kwanza, Ili kuleta wana wako kutoka mbali, Na fedha yao na dhahabu yao pamoja nao, Kwa ajili ya jina la Bwana, Mungu wako, Kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli, Kwa kuwa amekutukuza wewe. 10 Na wageni watajenga kuta zako, Na wafalme wao watakuhudumu; Maana katika ghadhabu yangu nalikupiga, Lakini katika upendeleo wangu nimekurehemu. 11 Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; Hayatafungwa mchana wala usiku; Ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa, Na wafalme wao wakiongozwa pamoja nao. 12 Kwa maana kila taifa na ufalme wa watu Wasiotaka kukutumikia wataangamia; Naam, mataifa hayo wataharibiwa kabisa. 13 Utukufu wa Lebanoni utakujia wewe, Mberoshi na mtidhari na mteashuri pamoja; Ili kupapamba mahali pangu patakatifu, Nami nitapatukuza mahali pa miguu yangu. 14 Na wana wa watu wale waliokutesa Watakuja kwako na kukuinamia; Nao wote waliokudharau Watajiinamisha hata nyayo za miguu yako; Nao watakuita, Mji wa Bwana, Sayuni wa Mtakatifu wa Israeli. 15 Na kwa kuwa umeachwa na kuchukiwa, Hata ikawa hapana mtu aliyepita ndani yako, Nitakufanya kuwa fahari ya milele, Furaha ya vizazi vingi. 16 Utanyonya maziwa ya mataifa, Utanyonya matiti ya wafalme; Nawe utajua ya kuwa mimi, Bwana, ni mwokozi wako, Na mkombozi wako, Mwenye enzi wa Yakobo. 17 Badala ya shaba nitaleta dhahabu, Na badala; ya chuma nitaleta fedha, Na badala ya mti, shaba, Na badala ya mawe, chuma; Tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, Na hao wakutozao fedha kuwa haki. 18 Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, Ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako; Bali utaziita kuta zako, Wokovu, Na malango yako, Sifa. 19 Jua halitakuwa nuru yako tena wakati wa mchana, Wala mwezi hautakupa nuru kwa mwangaza wake; Bali Bwana atakuwa nuru ya milele kwako, Na Mungu wako atakuwa utukufu wako. 20 Jua lako halitashuka tena, Wala mwezi wako hautajitenga; Kwa kuwa Bwana mwenyewe atakuwa nuru yako ya milele; Na siku za kuomboleza kwako zitakoma. 21 Watu wako nao watakuwa wenye haki wote, Nao watairithi nchi milele; 22 Mdogo atakuwa elfu, Na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, Bwana, nitayahimiza hayo wakati wake.

Isaya 61

1 Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao. 2 Kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao; 3 kuwaagizia hao waliao katika Sayuni, wapewe taji ya maua badala ya majivu, mafuta ya furaha badala ya maombolezo, vazi la sifa badala ya roho nzito; wapate kuitwa miti ya haki, iliyopandwa na Bwana, ili atukuzwe. 4 Nao watajenga mahali pa kale palipoharibiwa, watapainua mahali palipokuwa ukiwa zamani, watatengeneza miji iliyoharibiwa, mahali palipoachwa kizazi baada ya kizazi. 5 Na wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu. 6 Bali ninyi mtaitwa makuhani wa Bwana; watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu; mtakula utajiri wa mataifa, na kujisifia utukufu wao. 7 Badala ya aibu yenu mtapata maradufu, na badala ya fedheha wataifurahia sehemu yao; basi katika nchi yao watamiliki maradufu; furaha yao itakuwa ya milele. 8 Maana mimi, Bwana, naipenda hukumu ya haki, nauchukia wivi na uovu; nami nitawalipa malipo katika kweli, nitaagana nao agano la milele. 9 Na kizazi chao kitajulikana katika mataifa, na uzao wao katika kabila za watu; wote wawaonao watakiri ya kuwa wao ni kizazi kilichobarikiwa na Bwana. 10 Nitafurahi sana katika Bwana, nafsi yangu itashangilia katika Mungu wangu; maana amenivika mavazi ya wokovu, amenifunika vazi la haki, kama bwana arusi ajipambavyo kwa kilemba cha maua, na kama bibi arusi ajipambavyo kwa vyombo vya dhahabu. 11 Maana kama nchi itoavyo machipuko yake, na kama bustani ioteshavyo vitu vilivyopandwa ndani yake; ndivyo Bwana MUNGU atakavyootesha haki na sifa mbele ya mataifa yote.

Isaya 62

1 Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. 2 Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. 3 Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako. 4 Hutaitwa tena Aliyeachwa, wala nchi yako haitaitwa tena, Ukiwa; bali utaitwa Hefsiba; na nchi yako Beula;kwa kuwa Bwana anakufurahia,na nchi yako itaolewa. 5 Maana kama vile kijana amwoavyo mwanamwali, ndivyo wana wako watakavyokuoa wewe; na kama vile bwana arusi amfurahiavyo bibi arusi, ndivyo Mungu wako atakavyokufurahia wewe. 6 Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, Ee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala usiku; ninyi wenye kumkumbusha Bwana, msiwe na kimya; 7 wala msimwache akae kimya, mpaka atakapoufanya imara Yerusalemu, na kuufanya kuwa sifa duniani. 8 Bwana ameapa kwa mkono wake wa kuume, na kwa mkono wa nguvu zake, Hakika sitawapa adui zako nafaka yako tena kuwa chakula chao; wala wageni hawatakunywa divai yako, uliyoifanyia kazi. 9 Lakini walioivuna, ndio watakaoila, na kumhimidi Bwana; na walioichuma, ndio watakaoinywa, ndani ya nyua za patakatifu pangu. 10 Piteni, piteni, katika malango; Itengenezeni njia ya watu; Tutieni, tutieni barabara; toeni mawe yake; Twekeni bendera kwa ajili ya kabila za watu. 11 Tazama, Bwana ametangaza habari mpaka mwisho wa dunia, Mwambieni binti Sayuni, Tazama, wokovu wako unakuja; Tazama, thawabu yake i pamoja naye, Na malipo yake yako mbele zake. 12 Nao watawaita, Watu watakatifu, Waliokombolewa na Bwana; Nawe utaitwa, Aliyetafutwa, Mji usioachwa.

Isaya 63

1 Ni nani huyu atokaye Edomu, Mwenye mavazi ya kutiwa damu kutoka Bosra? Huyu aliye na nguo za fahari, Anayekwenda katika ukuu wa uweza wake? 2 Kwani mavazi yako kuwa mekundu, Na nguo zako kama za mtu akanyagaye zabibu? 3 Nalikanyaga shinikizoni peke yangu; Wala katika watu hakuwapo mtu pamoja nami; Naam, naliwakanyaga kwa hasira yangu, Naliwaponda kwa ghadhabu yangu; Na mavazi yangu yametiwa madoa kwa damu yao, Nami nimezichafua nguo zangu zote. 4 Maana siku ya kisasi ilikuwamo moyoni mwangu, Na mwaka wao niliowakomboa umewadia. 5 Nikatazama, wala hakuna wa kusaidia; Nikashangaa kwa kuwa hakuna mwenye kutegemeza; Basi, mkono wangu mwenyewe uliniletea wokovu, Ghadhabu yangu ndiyo iliyonitegemeza. 6 Nikazikanyaga kabila za watu kwa hasira yangu, Nikawalevya kwa ghadhabu yangu, Nami nikaimwaga damu yao chini. 7 Nitautaja wema wa Bwana, sifa za Bwana kwa yote aliyotukirimia Bwana; na wingi wa wema wake kwa nyumba ya Israeli, aliowakirimia kwa rehema zake, na kwa wingi wa wema wake. 8 Maana alisema, Hakika ndio watu wangu hawa, wana wasio na hila; akawa Mwokozi wao. 9 Katika mateso yao yote yeye aliteswa, na malaika wa uso wake akawaokoa; kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe; akawainua, akawachukua siku zote za kale. 10 Lakini wakaasi, wakamhuzunisha Roho yake Mtakatifu; kwa hiyo akawageukia, akawa adui, akapigana nao. 11 Ndipo alipozikumbuka siku za kale, za Musa, na watu wake, akisema, Yuko wapi yeye aliyewapandisha toka baharini pamoja na wachungaji wa kundi lake? Yuko wapi yeye aliyetia kati yao Roho yake Mtakatifu? 12 Aliyewaongoza kwa mkono wake mtukufu, kwa mkono wa kuume wa Musa? Aliyeyatenga maji mbele yao, ili ajifanyie jina la milele? 13 Aliyewaongoza vilindini, kama farasi jangwani, wasijikwae? 14 Kama ng'ombe washukao bondeni, Roho ya Bwana akawastarehesha; ndivyo ulivyowaongoza watu wako, ili ujifanyie jina lenye utukufu. 15 Tazama toka mbinguni, ukaone toka makao ya utukufu wako na fahari yako; uko wapi wivu wako, na uweza wako? Shauku ya moyo wako, na huruma zako zimezuiliwa kwangu. 16 Maana wewe ndiwe Baba yetu, ijapokuwa Ibrahimu hatujui, wala Israeli hatukiri; wewe, Bwana, ndiwe Baba yetu, mkombozi wetu tangu milele ndilo jina lako. 17 Ee Bwana, mbona umetukosesha njia zako, ukatufanyiza kuwa na mioyo migumu hata tusikuogope? Urudi kwa ajili ya watumishi wako, kabila za urithi wako. 18 Watu wako watakatifu waliumiliki kwa kitambo tu; adui zetu wamepakanyaga patakatifu pako. 19 Tumekuwa kama watu usiowamiliki kamwe; kama watu wasioitwa kwa Jina lako.

Isaya 64

1 Laiti ungepasua mbingu, na kushuka, ili milima iteteme mbele zako; 2 kama vile moto uchomapo vichaka, na moto uchemshapo maji; ili kuwajulisha adui zako jina lako, mataifa wakatetemeke mbele zako! 3 Ulipofanya mambo ya kutisha tusiyoyatazamia, ulishuka, milima ikatetema mbele zako. 4 Maana tangu zamani za kale watu hawakusikia, wala kufahamu kwa masikio, wala jicho halikuona Mungu, ila wewe, atendaye mambo kwa ajili yake amngojaye. 5 Wewe wamlaki yeye afurahiaye yaliyo haki na kuyatenda, watu wale wakukumbukao katika njia zako; tazama, ulikuwa na hasira, nasi tulitenda dhambi; tumekuwa katika mambo haya muda mwingi; nasi, je! Tutaokolewa? 6 Kwa maana sisi sote tumekuwa kama mtu aliye mchafu, na matendo yetu yote ya haki yamekuwa kama nguo iliyotiwa unajisi; sisi sote twanyauka kama jani, na maovu yetu yatuondoa, kama upepo uondoavyo. 7 Tena hapana aliitiaye jina lako, ajitahidiye akushike; kwa kuwa umetuficha uso wako, nawe umetukomesha kwa njia ya maovu yetu. 8 Lakini sasa, Ee Bwana, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu; sisi sote tu kazi ya mikono yako. 9 Ee Bwana, usione hasira nyingi, wala usiukumbuke uovu siku zote; tazama, angalia, twakusihi, sisi sote tu watu wako. 10 Miji yako mitakatifu imekuwa jangwa, Sayuni umekuwa jangwa, Yerusalemu umekuwa ukiwa. 11 Nyumba yetu takatifu, nzuri, walimokusifu baba zetu, imeteketea moto; vitu vyetu vyote vyenye kupendeza vimeharibika. 12 Utajizuia usiyaangalie mambo haya, Ee Bwana? Utanyamaza, na kututesa sana?

Isaya 65

1 Watu wasionitaka wanauliza habari zangu; nimeonekana na hao wasionitafuta; naliliambia taifa lisiloitwa kwa jina langu, 2 Nitazameni, nitazameni. Mchana kutwa nimewanyoshea mikono yangu watu walioasi, watu waendao katika njia isiyo njema, wakifuata mawazo yao wenyewe; 3 watu wanikasirishao mbele za uso wangu daima, wakitoa dhabihu katika bustani zao, na kufukiza uvumba juu ya matofali; 4 waketio kati ya makaburi, na kulala katika mahali pao pa siri; walao nyama ya nguruwe, na mchuzi wa vitu vinichukizavyo u katika vyombo vyao; 5 watu wasemao, Simama peke yako, usinikaribie mimi, kwa maana mimi ni mtakatifu kuliko wewe; watu hao ni moshi puani mwangu, moto uwakao mchana kutwa. 6 Tazama, neno hili limeandikwa mbele zangu. Sitanyamaza, lakini nitalipa, naam, mimi nitawalipa ujira wao vifuani mwao; 7 maovu yenu na maovu ya baba zenu pamoja, asema Bwana, ninyi mliofukiza uvumba juu ya milima, na kunitukana juu ya vilima; basi, kwa ajili ya hayo nitawapimia kwanza kazi yao vifuani mwao. 8 Bwana asema hivi, Kama vile divai mpya ipatikanavyo katika kichala, na mtu mmoja husema, Usikiharibu kwa maana mna baraka ndani yake; ndivyo nitakavyotenda kwa ajili ya watumishi wangu, ili nisiwaharibu wote. 9 Nami nitaleta uzao toka Yakobo, na mrithi wa milima yangu toka Yuda, na mteule wangu atairithi, na watumishi wangu watakaa huko. 10 Na Sharoni itakuwa zizi la makundi ya kondoo, na bonde la Akori mahali pa kulala makundi ya ng'ombe, kwa ajili ya watu wangu walionitafuta. 11 Bali ninyi mmwachao Bwana, na kuusahau mlima wangu mtakatifu, na kuandika meza kwa ajili ya Bahati, na kuijazia Ajali vyombo vya divai iliyochanganyika; 12 mimi nitawaandikia kuuawa kwa upanga, na ninyi nyote mtainama ili kuchinjwa; kwa sababu nilipoita hamkuitika; niliponena, hamkusikia; bali mlitenda yaliyo mabaya machoni pangu, mlichagua mambo nisiyoyafurahia. 13 Kwa hiyo Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, watumishi wangu watakula, bali ninyi mtaona njaa; tazama, watumishi wangu watakunywa, bali ninyi mtaona kiu; tazama, watumishi wangu watafurahi, bali ninyi mtatahayarika; 14 tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo, bali ninyi mtalia kwa huzuni ya moyo; mtapiga kelele kwa sababu ya uchungu wa roho zenu. 15 Nanyi mtaliacha jina lenu kuwa laana kwa wateule wangu. Na Bwana MUNGU atakuua; naye atawaita watumishi wake kwa jina lingine. 16 Hata itakuwa yeye atakayejibariki duniani, atajibariki kwa Mungu wa kweli; naye atakayeapa duniani, ataapa kwa Mungu wa kweli. Kwa kuwa taabu za kwanza zimesahauliwa, na kwa kuwa zimefichwa machoni pangu. 17 Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. 18 Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. 19 Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. 20 Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa. 21 Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. 22 Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. 23 Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na Bwana, na watoto wao pamoja nao. 24 Na itakuwa ya kwamba, kabla hawajaomba, nitajibu; na wakiwa katika kunena, nitasikia. 25 Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng'ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema Bwana.

Isaya 66

1 Bwana asema hivi, Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu; mtanijengea nyumba ya namna gani? Na mahali pangu pa kupumzikia ni mahali gani? 2 Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu. 3 Yeye achinjaye ng'ombe ni kama yeye amwuaye mtu; na yeye atoaye dhabihu ya mwana-kondoo ni kama yeye avunjaye shingo ya mbwa; na yeye atoaye matoleo ni kama yeye atoaye damu ya nguruwe; na yeye afukizaye uvumba ni kama yeye abarikiye sanamu; naam, wamezichagua njia zao wenyewe, na nafsi zao zafurahia machukizo yao. 4 Mimi nami nitachagua mapigo yao, nitaleta hofu zao juu yao; kwa sababu nilipoita, hawakuitika; na niliponena, hawakusikia; bali walifanya yaliyo maovu machoni pangu, na kuyachagua nisiyoyafurahia. 5 Lisikilizeni neno la Bwana, ninyi mtetemekao kwa sababu ya neno lake; Ndugu zenu wawachukiao ninyi, waliowatupa kwa ajili ya jina langu, wamesema, Na atukuzwe Bwana, tupate kuiona furaha yenu; lakini watatahayarika. 6 Sauti ya fujo itokayo mjini! Sauti itokayo hekaluni! Sauti ya Bwana awalipaye adui zake adhabu! 7 Kabla hajaona utungu alizaa; Kabla maumivu yake hayajampata, Alizaa mtoto mwanamume. 8 Ni nani aliyesikia neno kama hili? Ni nani aliyeona mambo kama haya? Je! Nchi yaweza kuzaliwa siku moja? Taifa laweza kuzaliwa mara? Maana Sayuni, mara alipoona utungu, Alizaa watoto wake. 9 Je! Mimi nilete wana karibu na kuzaliwa, nisizalishe? Asema Bwana; mimi nizalishaye, je! Nilifunge tumbo? Asema Mungu wako. 10 Furahini pamoja na Yerusalemu, shangilieni kwa ajili yake, ninyi nyote mmpendao; furahini pamoja naye kwa furaha, ninyi nyote mliao kwa ajili yake; 11 mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake, mpate kukama, na kufurahiwa kwa wingi wa utukufu wake. 12 Maana Bwana asema hivi, Tazama, nitamwelekezea amani kama mto, na utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho, nanyi mtapata kunyonya; mtabebwa; na juu ya magoti mtabembelezwa. 13 Mfano wa mtu ambaye mama yake amfariji, ndivyo nitakavyowafariji ninyi; nanyi mtafarijiwa katika Yerusalemu. 14 Nanyi mtaona, na mioyo yenu itafurahi, na mifupa yenu itasitawi kama majani mabichi; na mkono wa Bwana utajulikana, uwaelekeao watumishi wake, naye atawaonea adui zake ghadhabu. 15 Maana Bwana atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto. 16 Kwa maana Bwana atateta na wote wenye mwili, kwa moto na kwa upanga wake; nao watakaouawa na Bwana watakuwa wengi. 17 Watu wale wajitakasao, na kujisafisha katika bustani, nyuma yake aliye katikati; wakila nyama ya nguruwe, na machukizo, na panya; watakoma pamoja, asema Bwana. 18 Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu. 19 Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa. 20 Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka kwa Bwana, juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema Bwana; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka yao nyumbani kwa Bwana katika chombo safi. 21 Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi, asema Bwana. 22 Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema Bwana, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa. 23 Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema Bwana. 24 Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.

Yeremia 1

1 Maneno ya Yeremia, mwana wa Hilkia, mmoja wa makuhani waliokuwa katika Anathothi, katika nchi ya Benyamini; 2 ambaye neno la Bwana lilimjia katika siku za Yosia, mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda, katika mwaka wa kumi na tatu wa kumiliki kwake. 3 Tena lilikuja siku za Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, hata mwisho wa mwaka wa kumi na mmoja wa Sedekia, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda; hata wakati ulipochukuliwa mateka Yerusalemu, katika mwezi wa tano. 4 Neno la Bwana lilinijia, kusema, 5 Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa. 6 Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto. 7 Lakini Bwana akaniambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. 8 Usiogope kwa sababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema Bwana. 9 Ndipo Bwana akaunyosha mkono wake, akanigusa kinywa changu; Bwana akaniambia, Tazama, nimetia maneno yangu kinywani mwako; 10 angalia, nimekuweka leo juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung'oa, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza; ili kujenga na kupanda. 11 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, Yeremia, waona nini? Nikasema, Naona ufito wa mlozi. 12 Ndipo Bwana akaniambia, Umeona vema, kwa maana ninaliangalia neno langu, ili nilitimize. 13 Neno la Bwana likanijia mara ya pili, kusema, Waona nini? Nikasema, Naona sufuria lenye maji yatokotayo, na mdomo wake unaelekea toka upande wa kaskazini. 14 Ndipo Bwana akaniambia, Toka kaskazini mabaya yatatokea, na kuwapata watu wote wakaao katika nchi hii. 15 Kwa kuwa, tazama, nitaziita jamaa zote za falme za kaskazini, asema Bwana; nao watakuja, na kuweka kila mtu kiti chake cha enzi mbele ya mahali pa kuingilia malango ya Yerusalemu, na kuzielekea kuta zake pande zote, na kuielekea miji yote ya Yuda. 16 Nami nitatamka hukumu zangu juu yao kwa habari ya uovu wao wote; kwa kuwa wameniacha mimi, wakaifukizia uvumba miungu mingine, wakaziabudu kazi za mikono yao wenyewe. 17 Haya basi, wewe jifunge viuno, ukaondoke ukawaambie maneno yote niliyokuamuru; usifadhaike kwa ajili yao, nisije nikakufadhaisha wewe mbele yao. 18 Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalme wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii. 19 Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema Bwana, ili nikuokoe.

Yeremia 2

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Enenda ukalie masikioni mwa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Nakukumbuka, hisani ya ujana wako, upendo wa wakati wa uposo wako; Jinsi ulivyonifuata huko jangwani, katika nchi isiyopandwa mbegu. 3 Israeli walikuwa utakatifu kwa Bwana; malimbuko ya uzao wake; Wote watakaomla watakuwa na hatia; uovu utawajilia; asema Bwana. 4 Lisikieni neno la Bwana, ninyi nyumba ya Yakobo, na ninyi, jamaa zote za nyumba ya Israeli. 5 Bwana asema hivi, Baba zenu waliona dhuluma gani kwangu, hata wakafarakana nami, wakafuata ubatili, nao wakawa ubatili? 6 Wala hawakusema, Yuko wapi Bwana, aliyetutoa katika nchi ya Misri; akatuongoza jangwani, katika nchi ya ukame na mashimo, katika nchi ya kiu na ya kivuli cha mauti, katika nchi ambayo ndani yake hapiti mtu, wala haikukaliwa na watu? 7 Nami nikawatia katika nchi ya shibe, mpate kula matunda yake na mema yake; lakini ninyi mlipoingia katika nchi ile, mliitia unajisi nchi yangu, na urithi wangu mliufanya kuwa chukizo. 8 Makuhani hawakusema, Yuko wapi Bwana? Wala wana-sheria hawakunijua; wachungaji nao waliniasi, nao manabii walitoa unabii kwa Baali, wakafuata mambo yasiyofaidia kitu. 9 Basi, kwa ajili ya hayo nitateta nanyi, asema Bwana, nami nitateta na watoto wa watoto wenu. 10 Maana, vukeni mpaka visiwa vya Kitimu, mkaone; tumeni watu waende Kedari, mkafikiri sana; mkaone kwamba jambo kama hili limekuwa wakati wo wote. 11 Je! Taifa wamebadili miungu yao, ingawa siyo miungu? Lakini watu wangu wameubadili utukufu wao kwa ajili ya kitu kisichofaidia. 12 Enyi mbingu, staajabuni kwa ajili ya jambo hili, mkaogope sana, na kuwa ukiwa sana, asema Bwana. 13 Kwa maana watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji. 14 Je! Israeli ni mtumwa? Je! Ni mzalia? mbona amekuwa mateka? 15 Wana-simba wamenguruma juu yake, wametoa sana sauti zao; Nao wameifanya nchi yake kuwa ukiwa; miji yake imeteketea, haina watu. 16 Tena wana wa Nofu na Tahpanesi wamevunja utosi wa kichwa chako. 17 Je! Hukujipatia mambo haya mwenyewe, kwa kuwa umemwacha Bwana, Mungu wako, alipokuongoza njiani? 18 Na sasa una nini utakayotenda katika njia iendayo Misri, kunywa maji ya Shihori? Au una nini utakayotenda katika njia iendayo Ashuru, kunywa maji ya ule Mto? 19 Uovu wako mwenyewe utakurudi, maasi yako yatakukaripia; ujue, basi, ukaone, ya kuwa ni jambo baya sana na uchungu, kuwa umemwacha Bwana, Mungu wako, na ya kuwa moyoni mwako hamna kunihofu, asema Bwana, Bwana wa majeshi. 20 Kwa maana tangu zamani wewe umeivunja nira yako, na kuvipasua vifungo vyako; ukasema, Mimi sitatumika; kwa maana juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi, umejiinamisha, ukafanya mambo ya ukahaba. 21 Nami nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, mbegu nzuri kabisa; umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu? 22 Maana ujapojiosha kwa magadi, na kujipatia sabuni nyingi, lakini uovu wako umeandikwa mbele zangu, asema Bwana MUNGU. 23 Wawezaje kusema, Sikutiwa unajisi, sikuwafuata Mabaali? Itazame njia yako bondeni, ujue uliyoyatenda; wewe u ngamia mwepesi, apitaye katika njia zake; 24 punda wa mwitu aliyeizoelea nyika, avutaye pumzi za upepo katika tamaa yake; katika wakati wake ni nani awezaye kumgeuza? Wote wamtafutao hawatajichokesha nafsi zao; katika mwezi wake watamwona. 25 Zuia mguu wako usikose kiatu, na koo yako isiwe na kiu; lakini wewe ulisema, Hapana matumaini kabisa; la, maana nimewapenda wageni, nami nitawafuata. 26 Kama mwivi aonavyo haya akamatwapo, ndivyo waonavyo haya nyumba ya Israeli; wao, na wafalme wao, na wakuu wao, na makuhani wao, na manabii wao; 27 waliambiao gogo la mti, Wewe u baba yangu; na kuliambia jiwe, Ndiwe uliyenizaa; kwa maana wamenipa mimi visogo, wala hawakunielekezea nyuso zao; lakini wakati wa taabu watasema, Simama ukatuokoe. 28 Lakini wako wapi miungu yako ulioifanya? Na wasimame hao, kama wakiweza kukuokoa wakati wa taabu yako; kwa maana hesabu ya miungu yako ni sawasawa na hesabu ya miji yako, Ee Yuda. 29 Mbona mnataka kuteta nami? Ninyi nyote mmeniasi, asema Bwana. 30 Nimewapiga watoto wako bure; hawakukubali kurudiwa; upanga wenu wenyewe umewala manabii wako, kama simba aharibuye. 31 Ee kizazi litazameni neno la Bwana. Je! Nimekuwa jangwa kwa Israeli? Au nchi yenye giza kuu? Mbona watu wangu wanasema, Sisi tumetoroka, hatutaki kuja kwako tena? 32 Je! Mwanamwali aweza kusahau mapambo yake, au bibi arusi mavazi yake? Lakini watu wangu wamenisahau mimi kwa muda wa siku zisizo na hesabu. 33 Jinsi ulivyoitengeneza njia yako ili kutafuta mapenzi! Kwa sababu hiyo hata wanawake wabaya umewafundisha njia zako. 34 Tena katika pindo za nguo zako imeonekana damu ya roho zao maskini wasio na hatia; sikuiona penye mahali palipobomoka, lakini naliiona juu ya hawa wote. 35 Lakini ulisema, Sina hatia mimi; bila shaka hasira yake imegeuka na kuniacha. Tazama, nitaingia hukumuni pamoja nawe, kwa sababu unasema, Sikutenda dhambi mimi. 36 Mbona unatanga-tanga hivi upate kugeuza mwendo wako? Utaona haya kwa ajili ya Misri pia, kama ulivyoona haya kwa ajili ya Ashuru. 37 Hata kwake pia utatoka, na mikono yako juu ya kichwa chako; kwa maana Bwana amewakataa uliowakimbilia, wala hutafanikiwa katika hao.

Yeremia 3

1 Watu husema, Mtu akimwacha mkewe, naye akienda zake, akawa mke wa mtu mwingine, je! Mtu huyo atamrudia tena? Je! Nchi hiyo haitatiwa unajisi? Lakini wewe umefanya mambo ya ukahaba na wapenzi wengi; nawe, je! Utanirudia mimi? Asema Bwana. 2 Inua macho yako, ukavitazame vilele vya milima, ukaone; pa wapi mahali ambapo hawakulala nawe? Kando ya njia umeketi ili kuwangojea, kama vile Mwarabu jangwani; nawe umeitia nchi unajisi kwa ukahaba wako na uovu wako. 3 Kwa sababu hiyo manyunyu yamezuiliwa, wala hapakuwa na mvua ya vuli; hata hivyo ulikuwa na kipaji cha uso cha kahaba, ulikataa kutahayarika. 4 Je, tokea wakati huu hutanililia, Ee Baba yangu, wewe u kiongozi wa ujana wangu? 5 Je! Ataishika hasira yake hata milele? Ataishika hata mwisho? Tazama, umesema hivyo, bali umetenda mambo mabaya, umefuata njia yako mwenyewe. 6 Tena, Bwana akaniambia siku za mfalme Yosia, Je! Umeyaona aliyotenda Israeli mwenye kuasi? Amepanda juu ya kila mlima mrefu, akafanya huko mambo ya ukahaba, tena, chini ya kila mti wenye majani mabichi. 7 Nami nalisema baada ya yeye kuyatenda hayo yote, Atanirudia mimi, lakini hakurudi; na dada yake, Yuda mwenye hiana, akayaona hayo. 8 Nami nikaona, wakati nilipokuwa nimemwacha Israeli mwenye kuasi, nikampa hati ya talaka kwa sababu hiyo ya kuzini, dada yake, Yuda mwenye hiana, hakufanya hofu; bali yeye naye akaenda akafanya mambo ya ukahaba. 9 Hata ikawa, kwa sababu alikuwa mwepesi wa kufanya ukahaba, nchi ikatiwa unajisi, naye akazini na mawe na miti. 10 Na pamoja na hayo yote dada yake, Yuda mwenye hiana, hajanirudia mimi kwa moyo wake wote, bali kwa unafiki, asema Bwana. 11 Bwana, akaniambia, Israeli mwenye kuasi amejionyesha kuwa mwenye haki kuliko Yuda mwenye hiana. 12 Enenda, ukatangaze maneno haya kuelekea upande wa kaskazini, ukaseme, Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi, asema Bwana; sitakutazama kwa hasira; maana mimi ni mwenye rehema, asema Bwana, sitashika hasira hata milele. 13 Ungama uovu wako tu; ya kwamba umemwasi Bwana, Mungu wako, na njia zako zimekuwa nyingi kuwaendea wageni chini ya kila mti wenye majani mabichi, wala hamkuitii sauti yangu, asema Bwana. 14 Rudini, enyi watoto wenye kuasi, asema Bwana; maana mimi ni mume wenu; nami nitatwaa mtu mmoja wa mji mmoja, na wawili wa jamaa moja, nami nitawaleta hata Sayuni; 15 nami nitawapa ninyi wachungaji wanipendezao moyo wangu, watakaowalisha kwa maarifa na fahamu. 16 Kisha itakuwa, mtakapoongezeka na kuwa wengi katika nchi hiyo, asema Bwana, siku zile hawatasema tena, Sanduku la agano la Bwana; wala halitaingia moyoni; wala hawatalikumbuka, wala hawatalizuru, wala hayatafanyika hayo tena. 17 Wakati ule watauita Yerusalemu kiti cha enzi cha Bwana; na mataifa yote watakusanyika huko Yerusalemu, kwa ajili ya jina la Bwana; wala hawatakwenda tena kwa ukaidi wa moyo wao mbaya. 18 Siku zile nyumba ya Yuda watakwenda pamoja na nyumba ya Israeli, nao watakuja pamoja, kutoka nchi ya kaskazini, mpaka nchi ile niliyowapa baba zenu iwe urithi wao. 19 Lakini mimi nalisema, Nitawezaje kukuweka pamoja na watoto, na kukupa nchi ipendezayo, urithi ulio mwema wa mataifa? Nami nikasema, Mtaniita, Baba yangu, wala hamtageuka na kuacha kunifuata. 20 Hakika kama vile mke amwachavyo mumewe kwa hiana, ndivyo mlivyonitenda mimi kwa hiana, Ee nyumba ya Israeli, asema Bwana. 21 Sauti inasikiwa juu ya vilele vya milima, ni kulia kwao na maombi yao wana wa Israeli; kwa kuwa wameipotosha njia yao, wamemsahau Bwana, Mungu wao. 22 Rudini, enyi watoto waasi, mimi nitaponya maasi yenu. Tazama, tumekuja kwako; maana wewe u Bwana, Mungu wetu. 23 Ni kweli, msaada haufai unaotazamiwa kutoka milimani, makutano yenye mshindo juu ya milima; ni kweli, wokovu wa Israeli ni katika Bwana, Mungu wetu. 24 Lakini kitu cha aibu kimeila kazi ya baba zetu tokea ujana wetu; makundi yao ya kondoo na ng'ombe, wana wao na binti zao. 25 Na tulale kwa aibu yetu, haya yetu na itufunike; kwa maana tumemwasi Bwana, Mungu wetu, sisi na baba zetu, tangu ujana wetu hata leo; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu.

Yeremia 4

1 Kama ukitaka kurudi, Ee Israeli, asema Bwana, utanirudia mimi; na kama ukitaka kuyaondoa machukizo yako, yasiwe mbele ya macho yangu, ndipo hutaondolewa; 2 nawe utaapa hivi, Kama Bwana aishivyo, katika kweli, na katika hukumu, na katika haki ndipo mataifa watajibariki katika yeye, nao watajitukuza katika yeye. 3 Maana Bwana awaambia hivi watu wa Yuda na Yerusalemu Ulimeni udongo katika konde zenu, wala msipande mbegu kati ya miiba. 4 Jitahirini kwa Bwana, mkaziondoe govi za mioyo yenu, enyi watu wa Yuda na wenyeji wa Yerusalemu; ghadhabu yangu isije ikatoka kama moto, ikawaka hata mtu asiweze kuizima, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu. 5 Tangazeni katika Yuda, hubirini katika Yerusalemu, na kusema, Pigeni baragumu katika nchi, pigeni kelele sana, na kusema, Jikusanyeni pamoja, tukaingie katika miji yenye boma. 6 Twekeni bendera kuelekea Sayuni; kimbieni mpate kuwa salama, msikawie; kwa maana nitaleta mabaya toka kaskazini, na maangamivu makuu. 7 Simba ametoka katika kichaka chake, ndiye aangamizaye mataifa; ameanza kushika njia, ametoka katika mahali pake; ili aifanye nchi yako kuwa ukiwa, miji yako ifanywe maganjo, asibaki mwenyeji ndani yake. 8 Kwa sababu hiyo jifungeni nguo za magunia; ombolezeni na kulia kwa uchungu; kwa maana hasira kali ya Bwana haikugeuka na kutuacha. 9 Na katika siku hiyo itakuwa, asema Bwana, moyo wa mfalme utapotea, na moyo wa wakuu wake; na makuhani watastaajabu, na manabii watashangaa. 10 Nami nikasema, Aa, Bwana MUNGU! Hakika umewadanganya sana watu hawa na Yerusalemu, ukisema, Mtakuwa na amani lakini upanga umeingia katika nafsi za watu. 11 Wakati ule watu hawa na Yerusalemu wataambiwa neno hili, Upepo wa moto utokao katika vilele vya nyikani visivyo na miti, ukimwelekea binti ya watu wangu, hauwi upepo wa kupepeta, wala upepo wa kutakasa; 12 ni upepo wa nguvu kuliko hizo utakaokuja kwa ajili yangu; sasa mimi nitatoa hukumu juu yao. 13 Tazama atapanda juu kama mawingu, na magari yake ya vita yatakuwa kama kisulisuli; farasi zake ni wepesi kuliko tai. Ole wetu, kwa sababu tumeharibika. 14 Ee Yerusalemu, jioshe moyo wako usiwe na uovu, upate kuokoka. Mawazo yako mabaya yatakaa ndani yako hata lini? 15 Maana sauti yatangaza habari toka Dani, yahubiri uovu toka vilima vya Efraimu; 16 Wapasheni mataifa habari; angalieni, hubirini juu ya Yerusalemu, ya kwamba walinzi wanatoka katika nchi ya mbali, wanatoa sauti yao juu ya miji ya Yuda. 17 Kama watu walindao shamba, wameuzunguka wauhusuru; kwa sababu ameniasi mimi, asema Bwana. 18 Njia yako na matendo yako yamekupatia haya; huu ndio uovu wako; kwa maana ni uchungu, hakika unafikilia hata moyo wako. 19 Mtima wangu, mtima wangu! Naumwa katika moyo wangu wa ndani; moyo wangu umefadhaika ndani yangu; siwezi kunyamaza; kwa sababu umesikia, Ee nafsi yangu, sauti ya tarumbeta, mshindo wa vita. 20 Uangamivu baada ya uangamivu umetangazwa; kwa maana nchi yote imeharibika; hema zangu zimetekwa nyara ghafula, na mapazia yangu katika dakika moja. 21 Niione bendera hata lini, na kuisikia sauti ya tarumbeta? 22 Kwa maana watu wangu ni wapumbavu, hawanijui; ni watoto waliopungukiwa na akili, wala hawana ufahamu; ni wenye akili katika kutenda mabaya, bali katika kutenda mema hawana maarifa. 23 Naliiangalia nchi, na tazama, ilikuwa ukiwa, haina watu; naliziangalia mbingu, nazo zilikuwa hazina nuru. 24 Naliiangalia milima, na tazama, ilitetemeka, na milima yote ilisogea huko na huko. 25 Nikaangalia, na tazama, hapakuwa na mtu hata mmoja, na ndege wote wa angani wamekwenda zao. 26 Nikaangalia, na tazama, shamba lililozaa sana limekuwa ukiwa, na miji yake yote ilikuwa imebomoka mbele za Bwana, na mbele za hasira yake kali. 27 Maana Bwana asema hivi, Nchi yote itakuwa ukiwa; lakini sitaikomesha kabisa. 28 Kwa ajili ya hayo nchi itaomboleza, na mbingu zitakuwa nyeusi; kwa sababu mimi nimeyanena haya, na kuyakusudia, wala sikujuta wala mimi sitarudi nyuma niyaache. 29 Mji mzima unakimbia, kwa sababu ya mshindo wa wapanda farasi na wenye pinde wanaingia vichakani, wanapanda juu ya majabali; kila mji umeachwa, hapana hata mtu mmoja akaaye ndani yake. 30 Na wewe, utakapotekwa, utafanyaje? Ujapojivika mavazi mekundu, ujapojipamba mapambo ya dhahabu, ujapojitia wanja machoni, unajifanya kuwa mzuri bure tu; wapenzi wako wanakudharau; wanakutafuta roho yako. 31 Kwa maana nimesikia sauti, kama sauti ya mwanamke wakati wa utungu wake, na sauti yake aumwaye, kama mwanamke azaaye mtoto wake wa kwanza, sauti ya binti Sayuni, atwetaye kupata pumzi, na kunyosha mikono yake, akisema, Ole wangu, sasa! Kwa maana roho yangu inazimia mbele ya wauaji.

Yeremia 5

1 Pigeni mbio huku na huku katika njia za Yerusalemu, mkaone sasa, na kujua, na kutafuta katika viwanja vyake, kwamba mwaweza kumpata mtu mmoja, kwamba yuko mtu mmoja awaye yote atendaye kwa haki, atafutaye uaminifu; nami nitausamehe mji huo. 2 Na wajaposema, Kama Bwana aishivyo, hakika waapa kwa uongo. 3 Ee Bwana, macho yako je! Hayaangalii uaminifu? Umewapiga, lakini hawakuhuzunika; umewakomesha, lakini wamekataa kurudiwa wamefanya nyuso zao kuwa ngumu kuliko mwamba wamekataa kurudi. 4 Ndipo nikasema, Hakika, hawa ni maskini; ni wajinga hawa; maana hawaijui njia ya Bwana, wala hukumu ya Mungu wao; 5 nitawaendea watu wakubwa, nami nitasema nao; kwa maana hao wanaijua njia ya Bwana, na hukumu ya Mungu wao. Bali hawa kwa nia moja wameivunja nira, na kuvikata vifungo. 6 Basi, kwa hiyo, simba atokaye mwituni atawaua, mbwa-mwitu wa jioni atawateka, chui ataivizia miji yao, kila mtu atokaye humo atararuliwa vipande vipande; kwa sababu makosa yao ni mengi, na kurudi nyuma kwao kumezidi. 7 Nawezaje kukusamehe? Watoto wako wameniacha mimi, na kuapa kwa hao ambao si miungu; nilipokuwa nimewashibisha chakula, walizini, wakakutana wengi pamoja katika nyumba za makahaba. 8 Walikuwa kama farasi walioshiba wakati wa asubuhi; kila mmoja akalia kwa kutamani mke wa mwenzake. 9 Je! Nisiwapatilize kwa sababu ya mambo hayo? Asema Bwana; na nafsi yangu, je! Nisijilipize kisasi juu ya taifa la namna hii? 10 Pandeni juu ya kuta zake mkaharibu, lakini msiharibu kabisa; ondoeni matawi yake; kwa maana si yake Bwana. 11 Maana nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda wamenitenda kwa hiana sana, asema Bwana. 12 Wamemkataa Bwana, na kusema, Si yeye; wala hayatatupata mabaya; wala hatutaona upanga wala njaa; 13 na manabii watakuwa upepo, wala neno lake halimo ndani yao; basi ndivyo watakavyotendwa. 14 Kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wa majeshi, asema hivi, Kwa sababu mnasema neno hili, tazama, nitafanya maneno yangu katika kinywa chako kuwa moto, na watu hawa kuwa kuni, nao moto utawala. 15 Angalia, nitaleta taifa juu yenu litokalo mbali sana, Ee nyumba ya Israeli, asema Bwana; ni taifa hodari, ni taifa la zamani sana, taifa ambalo hujui lugha yake, wala huyafahamu wasemayo. 16 Podo lao ni kaburi wazi, ni mashujaa wote pia. 17 Nao watakula mavuno yako, na mkate wako, ambao iliwapasa wana wako na binti zako kuula; watakula makundi yako ya kondoo na ya ng'ombe; watakula mizabibu yako na mitini yako; wataiharibu miji yako yenye boma, uliyokuwa ukiitumainia, naam, wataiharibu kwa upanga. 18 Lakini hata katika siku zile, asema Bwana, sitawakomesha ninyi kabisa. 19 Tena itakuwa mtakapouliza, Bwana ametutenda mambo hayo yote kwa sababu gani? Ndipo utakapowaambia, Vile vile kama ninyi mlivyoniacha mimi, na kuwatumikia miungu mingine katika nchi yenu wenyewe, ndivyo mtakavyowatumikia wageni katika nchi isiyo yenu. 20 Tangazeni neno hili katika nyumba ya Yakobo, litangazeni katika Yuda, kusema, 21 Sikilizeni neno hili, enyi watu wajinga msio na ufahamu; mlio na macho ila hamwoni; mlio na masikio ila hamsikii. 22 Je! Hamniogopi mimi? Asema Bwana; hamtatetemeka mbele za uso wangu; mimi niliyeweka mchanga kuwa mpaka wa bahari, kwa amri ya daima, isiweze kuupita? Mawimbi yake yajapoumuka-umuka, hayawezi kushinda nguvu; yajapovuma sana, hayawezi kuupita. 23 Lakini watu hawa wana moyo wa kuasi na ukaidi; wameasi, wamekwenda zao. 24 Wala hawasemi mioyoni mwao, Basi, na tumche Bwana, Mungu wetu, aletaye mvua, mvua ya mwaka, na mvua ya vuli, kwa wakati wake; na kutuwekea juma za mavuno zilizoamriwa. 25 Maovu yenu yameyageuza haya, na dhambi zenu zimewazuilia mema msiyapate. 26 Maana katika watu wangu wameonekana watu waovu; huotea kama vile watu wategao mitego; hutega mtego, na kunasa watu. 27 Kama tundu lijaavyo ndege, kadhalika nyumba zao zimejaa hila; kwa hiyo wamekuwa wakuu, wamepata mali. 28 Wamewanda sana, wang'aa; naam, wamepita kiasi kwa matendo maovu; hawatetei madai ya yatima, ili wapate kufanikiwa; wala hawaamui haki ya mhitaji. 29 Je! Nisiwapatilize kwa mambo hayo? Asema Bwana; na nafsi yangu, je! Nisijilipize kisasi juu ya taifa la namna hii? 30 Jambo la ajabu, la kuchukiza, limetokea katika nchi hii! 31 Manabii wanatabiri uongo, na makuhani wanatawala kwa msaada wa hao; na watu wangu wanapenda mambo yawe hivyo. Nanyi mtafanya nini mwisho wake?

Yeremia 6

1 Kimbieni mpate kuwa salama, enyi wana wa Benyamini; tokeni katika Yerusalemu, pigeni tarumbeta katika Tekoa, simamisheni ishara juu ya Beth-hakeremu; kwa maana mabaya yanachungulia toka kaskazini, na uharibifu mkuu. 2 Binti Sayuni aliye mzuri, mwororo, nitamkatilia mbali. 3 Wachungaji na makundi yao ya kondoo watamjilia; watapiga hema zao karibu naye pande zote; watalisha kila mmoja mahali pake. 4 Takaseni vita juu yake; inukeni, na tupande juu wakati wa adhuhuri. Ole wetu, kwa kuwa mchana umeanza kupungua, vivuli vya jioni vinazidi kuwa virefu. 5 Inukeni, na tupande juu wakati wa usiku, tukayaharibu majumba yake. 6 Maana Bwana wa majeshi asema hivi, Jikatieni miti, mfanyize boma juu ya Yerusalemu. Mji huu ni mji unaojiliwa; dhuluma tupu imo ndani yake. 7 Kama vile kisima kitoavyo maji yake, ndivyo utoavyo uovu wake; jeuri na kuharibu kwasikiwa ndani yake; ugonjwa na jeraha zi mbele zangu daima. 8 Uadhibishwe, Ee Yerusalemu, nafsi yangu, isije ikafarakana nawe; nisije nikakufanya ukiwa, nchi isiyokaliwa na watu. 9 Bwana wa majeshi asema hivi, Wataokota mabaki ya Israeli kama mzabibu; rudisha mkono wako ndani ya vikapu, kama mchuma zabibu. 10 Niseme na nani na kushuhudia, wapate kusikia? Tazama, sikio lao halikutahiriwa, wala hawawezi kusikiliza; tazama, neno la Bwana limekuwa matukano kwao; hawalifurahii. 11 Lakini nimejaa ghadhabu ya Bwana; nimechoka kwa kujizuia; imwageni juu ya watoto walio njiani, na juu ya kusanyiko la vijana pia; maana hata mume atatwaliwa pamoja na mkewe, mzee pamoja na yeye aliyetimiza siku zake. 12 Na nyumba zao zitakuwa mali za watu wengine, mashamba yao na wake zao pamoja; kwa kuwa nitaunyosha mkono wangu juu ya wenyeji wa nchi hii, asema Bwana. 13 Kwa maana, tangu aliye mdogo hata aliye mkubwa miongoni mwao, kila mmoja ni mtamanifu; na, tangu nabii hata kuhani, kila mmoja hutenda mambo ya udanganyifu. 14 Wameiponya jeraha ya watu wangu kwa juu juu tu, wakisema, Amani, Amani, wala hapana amani. 15 Je! Walitahayarika, walipokuwa wameunda machukizo? La, hawakutahayarika hata kidogo, wala hawakuweza kuona haya usoni; basi, wataanguka miongoni mwa hao waangukao; wakati nitakapowajilia wataangushwa chini, asema Bwana. 16 Bwana asema hivi, Simameni katika njia kuu, mkaone, mkaulize habari za mapito ya zamani, I wapi njia iliyo njema? Mkaende katika njia hiyo, nanyi mtajipatia raha katika nafsi zenu. Lakini walisema, Hatutaki kwenda katika njia hiyo. 17 Nami naliweka walinzi juu yenu, wakisema, Isikilizeni sauti ya tarumbeta; lakini walisema, Hatutaki kusikiliza. 18 Kwa sababu hiyo sikilizeni, enyi mataifa, mkajue, Ee kusanyiko, ni jambo gani litokealo kati yao. 19 Sikia, Ee nchi; tazama, nitaleta mabaya juu ya watu hawa, naam, matunda ya mawazo yao, kwa sababu hawakuyasikiliza maneno yangu; tena kwa habari ya sheria yangu, wameikataa. 20 Yafaa nini niletewe ubani kutoka Sheba, na uudi kutoka nchi iliyo mbali? Sadaka zenu za kuteketezwa hazikubaliwi, wala dhabihu zenu haziniridhii. 21 Basi, kwa hiyo, Bwana asema hivi, Tazama, nitaweka makwazo mbele ya watu hawa, na baba na wana wao watajikwaa pamoja; jirani ya mtu na rafiki yake watapotea. 22 Bwana asema hivi, Tazama, watu wanakuja, wakitoka katika nchi ya kaskazini; na taifa kubwa litaamshwa, litokalo katika pande za mwisho wa dunia. 23 Washika upinde na mkuki; ni wakatili, hawana huruma; sauti yao huvuma kama bahari, nao wamepanda farasi zao; kila mmoja kama mtu wa vita amejipanga juu yako, Ee binti Sayuni. 24 Tumesikia habari zake; mikono yetu inalegea; dhiki imetushika, na utungu kama wa mwanamke wakati wa kuzaa kwake. 25 Msitoke kwenda mashambani, wala msitembee njiani, kwa maana upanga wa adui uko huko; hofu ziko pande zote. 26 Ee binti wa watu wangu, ujivike nguo ya magunia, na kugaagaa katika majivu; fanya maombolezo, kama maombolezo kwa ajili ya mwana wa pekee, maombolezo ya uchungu mwingi; maana mwenye kuteka nyara atakuja juu yetu ghafula. 27 Nimekuweka uwe mnara na ngome kati ya watu wangu; upate kuijua njia yao na kuijaribu. 28 Ni waasi kupita kiasi wote pia, waendao huko na huko wakisingizia, ni shaba na chuma hao, hutenda dhuluma wote pia. 29 Mifuo inafukuta kwa nguvu; risasi tu inatoka katika moto huo; mfua fedha ameyeyusha bure tu; maana wabaya hawaondolewi mbali. 30 Watu watawaita taka za fedha, kwa sababu Bwana amewakataa.

Yeremia 7

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 2 Simama langoni pa nyumba ya Bwana, ukatangaze hapo neno hili, ukisema, Sikilizeni neno la Bwana, ninyi nyote wa Yuda, mnaoingia katika malango haya ili kumwabudu Bwana. 3 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, nami nitawakalisha ninyi mahali hapa. 4 Msitumainie maneno ya uongo, mkisema, Hekalu la Bwana, Hekalu la Bwana, Hekalu la Bwana ndiyo haya. 5 Maana kama mkitengeneza kabisa njia zenu na matendo yenu; kama mkihukumu hukumu ya haki kati ya mtu na jirani yake; 6 kama hamwonei mgeni, wala yatima, wala mjane, wala kumwaga damu isiyo na hatia mahali hapa, wala kuifuata miungu mingine kwa hasara yenu wenyewe; 7 ndipo nitakapowakalisha mahali hapa, katika nchi hii niliyowapa baba zenu, tokea zamani hata milele. 8 Angalieni, mnatumainia maneno ya uongo, yasiyoweza kufaidia. 9 Je! Mtaiba, na kuua, na kuzini, na kuapa kwa uongo, na kumfukizia Baali uvumba, na kuifuata miungu mingine ambayo hamkuijua; 10 kisha mtakuja na kusimama mbele zangu katika nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, na kusema, Tumepona; ili mpate kufanya machukizo hayo yote? 11 Je! Nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, imekuwa pango la wanyang'anyi machoni penu? Angalieni, mimi, naam, mimi, nimeliona jambo hili, asema Bwana. 12 Lakini enendeni sasa hata mahali pangu palipokuwapo katika Shilo, nilipolikalisha jina langu hapo kwanza, mkaone nilivyopatenda kwa sababu ya uovu wa watu wangu Israeli. 13 Na sasa, kwa sababu mmezifanya kazi hizi zote asema Bwana, nami nikasema nanyi, nikiamka mapema na kunena, lakini hamkusikia; nami nikawaita wala hamkuniitikia; 14 basi, nitaitenda nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, mnayoitumainia, na mahali hapa nilipowapa ninyi na baba zenu, kama nilivyopatenda Shilo. 15 Nami nitawatupa ninyi mbali na macho yangu, kama nilivyowatupa ndugu zenu wote, yaani, wazao wote wa Efraimu. 16 Basi, wewe usiwaombee watu hawa, wala usiwapazie sauti yako, wala kuwaombea dua, wala usinisihi kwa ajili yao; kwa maana sitakusikiliza. 17 Je! Huoni wanavyotenda katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu? 18 Watoto huokota kuni, na baba zao huwasha moto, na wanawake hukanda unga, ili kumfanyizia mikate malkia wa mbinguni, na kuwamiminia miungu mingine sadaka za kinywaji, wapate kunikasirisha mimi. 19 Je! Watu hawa wanikasirisha mimi? Asema Bwana; hawajikasirishi nafsi zao, na kuzitia haya nyuso zao wenyewe? 20 Kwa hiyo, Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa juu ya mahali hapa, juu ya wanadamu, na juu ya wanyama, na juu ya miti ya mashamba, na juu ya mazao ya nchi; nayo itateketea, isizimike. 21 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tieni sadaka zenu za kuteketezwa pamoja na dhabihu zenu, mkale nyama. 22 Maana sikusema na baba zenu, wala sikuwaamuru kwa habari za sadaka za kuteketezwa na dhabihu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri; 23 lakini naliwaamuru neno hili, nikisema, Sikilizeni sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu; mkaende katika njia ile yote nitakayowaamuru mpate kufanikiwa. 24 Lakini hawakusikiliza, wala kutega sikio lao, bali walikwenda kwa mashauri yao wenyewe, na kwa ushupavu wa mioyo yao mibaya, wakaenda nyuma wala si mbele. 25 Tokea siku ile baba zenu walipotoka katika nchi ya Misri hata leo, nimewatuma watumishi wangu wote manabii kwenu ninyi, nikiamka mapema kila siku, na kuwatuma. 26 Lakini hawakunisikiliza, wala kutega sikio lao; bali walifanya shingo yao kuwa ngumu; walitenda mabaya kuliko baba zao. 27 Nawe utawaambia maneno hayo yote; lakini hawatakusikiliza, nawe utawaita; lakini hawatakuitikia. 28 Nawe utawaambia, Taifa hili ndilo lisilosikiliza sauti ya Bwana, Mungu wao, wala kupokea mafundisho; uaminifu umepotea, umekatiliwa mbali na vinywa vyao. 29 Zikate nywele zako, Ee Yerusalemu, uzitupe, Ukafanye maombolezo juu ya vilele vya milima; Kwa maana Bwana amekikataa na kukitupa Kizazi cha ghadhabu yake. 30 Maana wana wa Yuda wametenda yaliyo maovu machoni pangu, asema Bwana; wameweka machukizo yao ndani ya nyumba hiyo, iitwayo kwa jina langu, hata kuitia unajisi. 31 Nao wamepajenga mahali palipoinuka pa Tofethi, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwateketeza wana wao na binti zao motoni; jambo ambalo mimi sikuliagiza, wala halikuingia moyoni mwangu. 32 Basi angalieni, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo katika siku hizo halitaitwa tena Tofethi, wala Bonde la mwana wa Hinomu bali litaitwa, Bonde la Machinjo; maana watazika watu katika Tofethi, hata hapatakuwapo mahali pa kuzika tena. 33 Na mizoga ya watu hawa itakuwa chakula cha ndege wa angani, na cha wanyama wa nchi; wala hapana mtu atakayewafukuza. 34 Ndipo katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, nitaikomesha sauti ya kicheko na sauti ya furaha, sauti ya bwana arusi na sauti ya bibi arusi; kwa maana nchi hiyo itakuwa ukiwa.

Yeremia 8

1 Wakati ule, asema Bwana, watatoa mifupa ya wafalme wa Yuda, na mifupa ya wakuu wake, na mifupa ya makuhani, na mifupa ya manabii na mifupa ya wenyeji wa Yerusalemu, itoke makaburini mwao; 2 nao wataitawanya mbele ya jua, na mwezi, na jeshi lote la mbinguni, walivyovipenda, na kuvitumikia, na kuandamana navyo, na kuvitafuta, na kuviabudu haitakusanywa pamoja tena, wala kuzikwa; itakuwa ni samadi juu ya uso wa nchi. 3 Na kufa kutachaguliwa kuliko kuishi na mabaki yote waliosalia katika jamaa hii mbovu, waliosalia kila mahali nilikowafukuza, asema Bwana wa majeshi. 4 Tena utawaambia, Bwana asema hivi, Je! Watu wataanguka, wasisimame tena? Je! Mtu atageuka aende zake, asirudi tena? 5 Mbona, basi, watu hawa wa Yerusalemu wamegeuka waende nyuma, wasikome kugeuka hivyo? Hushika udanganyifu sana, hukataa kurudi. 6 Nalisikiliza nikasikia, lakini walisema yasiyo sawa; hapana mtu aliyetubia maovu yake, akisema, Nimefanya nini? Kila mtu hurudia mwendo wake mwenyewe, kama farasi aendavyo kasi vitani. 7 Naam, koikoi angani ajua nyakati zake zilizoamriwa; na hua na mbayuwayu na korongo huangalia wakati wa kuja kwao; bali watu wangu hawazijui amri za Bwana. 8 Mwasemaje, Sisi tuna akili, na torati ya Bwana tunayo pamoja nasi? Lakini, tazama, kalamu yenye uongo ya waandishi imeifanya kuwa uongo. 9 Wenye hekima wametahayari, wamefadhaika na kushikwa; tazama, wamelikataa neno la Bwana, wana akili gani ndani yao? 10 Basi, kwa hiyo nitawapa watu wengine wake zao na mashamba yao nitawapa wale watakaowamiliki; maana kila mmoja wao, tangu aliye mdogo hata aliye mkubwa, ni mtamanifu; tangu nabii hata kuhani, kila mmoja hutenda mambo ya udanganyifu. 11 Kwa maana wameiponya jeraha ya binti ya watu wangu kwa juu-juu tu, wakisema, Amani, Amani, wala hapana amani. 12 Je! Walitahayarika, walipokuwa wametenda machukizo? La! Hawakutahayarika, wala hawakuweza kuona haya usoni; basi wataanguka miongoni mwao waangukao; wakati wa kujiliwa kwao wataangushwa chini, asema Bwana. 13 Nitawaangamiza kabisa, asema Bwana; hapana zabibu katika mizabibu, wala tini katika mitini, hata jani lake litanyauka; na vitu vile nilivyowapa vitawapotea. 14 Mbona tunakaa kimya? Jikusanyeni, tukaingie ndani ya miji yenye maboma, tukanyamaze humo kwa maana Bwana, Mungu wetu, ametunyamazisha, naye ametupa maji yenye uchungu tunywe, kwa sababu tumemwasi Bwana. 15 Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote; tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu! 16 Kutoka Dani kumesikiwa mkoromo wa farasi zake; nchi yote pia inatetemeka kwa sauti ya mlio wa farasi zake za vita; maana wamekuja, wamekula nchi na vyote vilivyomo; huo mji na wote wakaao ndani yake. 17 Maana, tazama, nitatuma nyoka, naam, fira, kati yenu, wasioweza kutumbuizwa kwa uganga; nao watawauma, asema Bwana. 18 Laiti ningeweza kujifariji, nisione huzuni! Moyo wangu umezimia ndani yangu. 19 Tazama, sauti ya kilio cha binti ya watu wangu, itokayo katika nchi iliyo mbali sana; Je! Bwana hayumo katika Sayuni? Mfalme wake hayumo ndani yake? Mbona wamenikasirisha kwa sanamu zao walizochonga, na kwa ubatili wa kigeni? 20 Mavuno yamepita, wakati wa hari umekwisha, wala sisi hatukuokoka. 21 Kwa sababu ya maumivu ya binti ya watu wangu nimeumia mimi; nimevaa kaniki; ushangao umenishika. 22 Je! Hapana zeri katika Gileadi? Huko hakuna tabibu? Mbona, basi, haijarejea afya ya binti ya watu wangu?

Yeremia 9

1 Laiti kichwa changu kingekuwa maji, na macho yangu kuwa chemchemi ya machozi, ili nipate kulia mchana na usiku kwa ajili yao waliouawa wa binti ya watu wangu! 2 Laiti ningekuwa na mahali pa kukaa jangwani, kibanda cha wasafiri; nipate kuwaacha watu wangu, na kuondoka kwao! Maana wao ni wazinzi, wote pia, mkutano wa watu wenye hiana. 3 Huupinda ulimi wao, kana kwamba ni upinde, ili kusema uongo; nao wamepata nguvu katika nchi, lakini si katika uaminifu; maana huendelea toka ubaya hata ubaya, wala hawanijui mimi, asema Bwana. 4 Jihadharini, kila mtu na jirani yake, wala msimtumaini ndugu awaye yote; maana kila ndugu atachongea, na kila jirani atakwenda huko na huko na kusingizia. 5 Nao watadanganya kila mtu jirani yake, wala hawatasema kweli; wameuzoeza ulimi wao kusema uongo; hujidhoofisha ili kutenda uovu. 6 Makao yako ya katikati ya hadaa; kwa hadaa wanakataa kunijua mimi, asema Bwana. 7 Basi, kwa hiyo Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama, nitawayeyusha na kuwajaribu; maana nisipotenda hivi, nitende nini kwa ajili ya binti ya watu wangu? 8 Ulimi wao ni mshale ufishao; husema maneno ya hadaa; mtu mmoja husema maneno ya amani na mwenzake kwa kinywa chake, lakini moyoni mwake humwotea. 9 Je! Nisiwapatilize kwa mambo hayo? Asema Bwana; na nafsi yangu je! Nisijilipize kisasi juu ya taifa la namna hii? 10 Kwa milima nitalia na kulalama, Na kwa malisho ya nyikani nitafanya maombolezo; Kwa sababu yameteketea, hata hapana apitaye, Wala hapana awezaye kusikia sauti ya ng'ombe; Ndege wa angani, na wanyama wa mwituni, Wamekimbia, wamekwenda zao. 11 Nami nitafanya Yerusalemu kuwa magofu, Makao ya mbweha; Nami nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, Isikaliwe na mtu awaye yote. 12 Ni nani aliye na hekima, apate kuelewa na haya? Tena ni nani ambaye kinywa cha Bwana kimesema naye, apate kuyatangaza? Nayo ni nini maana yake nchi hii kuharibika, na kuteketea kama nyika, asipite mtu? 13 Naye Bwana asema, Ni kwa sababu wameiacha sheria yangu niliyoweka mbele yao, wala hawakuitii sauti yangu, wala kuenenda katika hiyo; 14 bali wameenenda katika ushupavu wa mioyo yao wenyewe, na kuandamana na Mabaali, kama walivyofundishwa na baba zao. 15 Basi, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitawalisha pakanga, naam, watu hawa, nami nitawapa maji ya uchungu wayanywe. 16 Nami nitawatawanya kati ya mataifa, ambao wao hawakuwajua; wala baba zao, nami nitatuma upanga nyuma yao, hata nitakapowaangamiza kabisa. 17 Bwana wa majeshi asema hivi, Fikirini ninyi, mkawaite wanawake waombolezao, ili waje; mkatume na kuwaita wanawake wenye ustadi, ili waje; 18 na wafanye haraka na kutuombolezea, ili macho yetu yachuruzike machozi, na kope zetu zibubujike maji. 19 Maana sauti ya maombolezo imesikiwa toka Sayuni, Jinsi tulivyotekwa! tulivyofadhaika sana! Kwa sababu tumeiacha nchi, kwa kuwa wameangusha makao yetu. 20 Lakini lisikieni neno la Bwana, enyi wanawake, Na masikio yenu yapokee neno la kinywa chake; Mkawafundishe binti zenu kuomboleza, Na kila mmoja jirani yake kulia. 21 Kwa maana mauti imepandia madirishani mwetu, imeingia majumbani mwetu; Ipate kuwakatilia mbali watoto walio nje, na vijana katika njia kuu. 22 Nena, Bwana asema hivi, Mizoga ya watu itaanguka kama samadi juu ya mashamba, Na kama konzi ya ngano nyuma yake avunaye, wala hapana mtu atakayeikusanya. 23 Bwana asema hivi, Mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekima yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake; 24 bali ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni Bwana, nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo, asema Bwana, 25 Tazama, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapowaadhibu wote waliotahiriwa katika hali yao ya kutokutahiriwa; 26 Misri, na Yuda, na Edomu, na wana wa Amoni, na Moabu, na wote wenye kunyoa denge, wakaao nyikani; maana mataifa hayo yote hawana tohara, wala nyumba yote ya Israeli hawakutahiriwa mioyo yao.

Yeremia 10

1 Enyi nyumba ya Israeli, lisikieni neno awaambialo Bwana; 2 Bwana asema hivi, Msijifunze njia ya mataifa, wala msishangae kwa sababu ya ishara za mbinguni; maana mataifa hushangaa kwa sababu ya ishara hizo. 3 Maana desturi za watu hao ni ubatili, maana mtu mmoja hukata mti mwituni, kazi ya mikono ya fundi na shoka. 4 Huupamba kwa fedha na dhahabu; huukaza kwa misumari na nyundo, usitikisike. 5 Mfano wao ni mfano wa mtende, kazi ya cherehani, hawasemi; hawana budi kuchukuliwa, kwa sababu hawawezi kwenda. Usiwaogope; kwa maana hawawezi kutenda uovu, wala hawana uwezo wa kutenda mema. 6 Hapana hata mmoja aliye kama wewe, Ee Bwana; wewe ndiwe uliye mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza. 7 Ni nani asiyekucha wewe, Ee mfalme wa mataifa? Maana hii ni sifa yako wewe; kwa kuwa miongoni mwa wenye hekima wote wa mataifa, na katika hali yao ya enzi yote pia, hapana hata mmoja kama wewe. 8 Lakini wote pia huwa kama wanyama, ni wapumbavu. Haya ni maelezo ya sanamu, ni shina la mti tu. 9 Iko fedha iliyofuliwa ikawa mabamba, iliyoletwa kutoka Tarshishi, na dhahabu kutoka Ufazi, kazi ya stadi na ya mikono ya mfua dhahabu; mavazi yao ni rangi ya samawi na urujuani; hayo yote ni kazi ya mafundi yao. 10 Bali Bwana ndiye Mungu wa kweli; Ndiye Mungu aliye hai, Mfalme wa milele; Mbele za ghadhabu yake nchi yatetemeka, Wala mataifa hawawezi kustahimili hasira yake. 11 Mtawaambia hivi, Miungu hiyo isiyofanya mbingu na nchi, hiyo itaangamia katika nchi, nayo itatoweka chini ya mbingu. 12 Ameiumba dunia kwa uweza wake, Ameuthibitisha ulimwengu kwa hekima yake, Na kwa ufahamu wake amezitandika mbingu. 13 Atoapo sauti yake, pana mshindo wa maji mbinguni, Naye hupandisha mawingu toka ncha za nchi; Huifanyia mvua umeme, Huutoa upepo katika hazina zake. 14 Kila mtu amekuwa kama mnyama, hana maarifa; Kila mfua dhahabu amefedheheshwa na sanamu yake ya kuchonga; Maana sanamu yake ya kuyeyuka ni uongo, Wala hamna pumzi ndani yake. 15 Ni ubatili tu, ni kazi za udanganyifu; Wakati wa kujiliwa kwao watapotea. 16 Yeye, Fungu la Yakobo, siye kama hawa; Maana ndiye aliyeviumba vitu vyote; Na Israeli ni kabila ya urithi wake; Bwana wa majeshi ndilo jina lake. 17 Haya! Kusanya bidhaa yako katika nchi, wewe ukaaye katika mazingiwa. 18 Maana Bwana asema hivi, Tazama, wakati huu nitawatupa wenyeji wa nchi hii kama kwa kombeo, nitawataabisha, wapate kuona taabu. 19 Ole wangu, kwa sababu ya jeraha yangu! Pigo langu laumia; lakini nalisema, Kweli, ni huzuni yangu mimi, nami sina budi kuivumilia. 20 Hema yangu umetekwa nyara, kamba zangu zote zimekatika; watoto wangu wameniacha na kwenda zao, pia hawako. Hapana mtu atakayenitandikia tena hema yangu, na kuyatundika mapazia yangu. 21 Kwa sababu wachungaji wamekuwa kama wanyama, wala hawakuuliza kwa Bwana; basi hawakufanikiwa, na makundi yao yote yametawanyika. 22 Sauti imesikiwa, Tazama, inakuja; mshindo mkuu kutoka nchi ya kaskazini, ili kuifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, makao ya mbweha. 23 Ee Bwana, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu. 24 Ee Bwana, unirudi kwa haki; si kwa hasira yako, usije ukaniangamiza. 25 Hasira yako uwamwagie mataifa wasiokujua, na jamaa zao wasioliitia jina lako; kwa maana wamemla Yakobo, naam, wamemla kabisa na kumwangamiza, na kuyafanya makao yake kuwa ukiwa.

Yeremia 11

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 2 Yasikieni maneno ya maagano haya; ukaseme na watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu; 3 ukawaambie, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Na alaaniwe mtu asiyeyasikia maneno ya maagano haya, 4 niliyowaamuru baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, katika tanuru ya chuma, nikisema, Itiini sauti yangu, mkafanye sawasawa na yote niwaagizayo ninyi; ndivyo mtakavyokuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu; 5 ili nipate kukitimiza kiapo nilichowaapia baba zenu, kuwapa nchi ijaayo maziwa na asali, kama ilivyo leo hivi. Ndipo nikajibu, nikasema, Amina, Ee Bwana. 6 Naye Bwana akaniambia, Hubiri maneno haya yote katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, ukisema, Yasikieni maneno ya maagano haya, mkayafanye. 7 Kwa maana naliwashuhudia sana baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, hata leo, nikiamka mapema na kuwashuhudia, nikisema, Itiini sauti yangu. 8 Lakini hawakutii, wala kutega masikio yao, bali walikwenda kila mtu katika ushupavu wa moyo wake mbaya; kwa hiyo nimeleta juu yao maneno yote ya maagano haya, niliyowaamuru wayafanye; lakini hawakuyafanya. 9 Naye Bwana akaniambia, Fitina imeonekana katika watu wa Yuda, na katika wenyeji wa Yerusalemu. 10 Wameyarudia maovu ya baba zao, waliokataa kusikia maneno yangu; wamewafuata miungu mingine na kuwatumikia; nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda, wameyavunja maagano yangu niliyoyafanya na baba zao. 11 Basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitaleta mabaya juu yao, ambayo hawataweza kuyakimbia; nao watanililia, walakini sitawasikiliza. 12 Ndipo miji ya Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, watakwenda na kuwalilia miungu wawafukiziao uvumba; lakini hawatawaokoa hata kidogo wakati wa taabu yao. 13 Maana hesabu ya miungu yako, Ee Yuda, ni sawasawa na hesabu ya miji yako; na kama ilivyo hesabu ya njia za Yerusalemu, ndivyo mlivyosimamisha madhabahu za kitu kile cha aibu, madhabahu za kumfukizia Baali uvumba. 14 Basi, usiwaombee watu hawa, wala usipaze sauti yako, wala kuwaombea dua watu hawa; maana sitawasikia wakati watakaponililia kwa ajili ya taabu yao. 15 Mpenzi wangu afanya nini nyumbani mwangu, ikiwa amefanya uasherati? Je! Nadhiri zako na nyama takatifu zitakuondolea hatia? Ufanyapo maovu, ndipo uonapo furaha. 16 Bwana alikuita jina lako, Mzeituni wenye majani mabichi, mzuri, wenye matunda mema; kwa kelele za mshindo mkuu amewasha moto juu yake, na matawi yake yamevunjika. 17 Kwa maana Bwana wa majeshi, aliyekupanda, ametamka mabaya juu yako, kwa sababu ya maovu ya nyumba ya Israeli, na ya nyumba ya Yuda, waliyoyatenda juu ya nafsi zao wenyewe kwa kunikasirisha, wakimfukizia Baali uvumba. 18 Tena Bwana akanijulisha haya, nami nikayajua; ndipo uliponionyesha matendo yao. 19 Lakini mimi nalikuwa kama mwana-kondoo mpole, achukuliwaye kwenda kuchinjwa; wala sikujua ya kuwa wamefanya mashauri kinyume changu, wakisema, Na tuuharibu mti pamoja na matunda yake, na tumkatilie mbali atoke katika nchi ya walio hai, ili jina lake lisikumbukwe tena. 20 Lakini, Ee Bwana wa majeshi, uhukumuye haki, ujaribuye viuno na moyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu. 21 Basi, kwa hiyo, Bwana asema hivi, juu ya watu wa Anathothi, watakao uhai wako, wakisema, Hutafanya unabii kwa jina la Bwana, usije ukafa kwa mkono wetu. 22 Kwa sababu hiyo Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama, nitawaadhibu watu hawa; vijana watakufa kwa upanga; wana wao na binti zao watakufa kwa njaa; 23 wala hapatakuwa na mtu atakayesalia kwao; maana nitaleta mabaya juu ya watu wa Anathothi, mwaka wa kujiliwa kwao.

Yeremia 12

1 Wewe u mwenye haki, Ee Bwana, nitetapo nawe, lakini nitasema nawe katika habari ya haki. Mbona njia ya wabaya inasitawi? Mbona wote watendao hila wanakaa salama? 2 Umewapanda, naam, wametia mizizi, wanakua, naam, wanazaa matunda; katika vinywa vyao u karibu, bali katika mioyo yao u mbali. 3 Lakini wewe, Bwana, wanijua; umeniona, umeujaribu moyo wangu, jinsi unavyokuelekea; uwakokote kama kondoo waendao kuchinjwa, ukawaweke tayari kwa siku ya kuchinjwa. 4 Hata lini itaomboleza nchi, na kukauka majani ya nchi yote? Kwa ajili ya mabaya yao wakaao ndani yake, wanyama wameangamia na ndege pia; kwa sababu walisema, Hatauona mwisho wetu. 5 Ikiwa umepiga mbio pamoja na hao waendao kwa miguu, nao wamekuchosha, basi wawezaje kushindana na farasi? Na ujapokuwa katika nchi ya amani u salama, lakini utafanyaje hapo katika kiburi cha Yordani? 6 Kwa maana hata ndugu zako, na nyumba ya baba yako, wamekutenda mambo ya hila; naam, wamepiga kelele nyuma yako; usiwasadiki, wajapokuambia maneno mazuri. 7 Nimeiacha nyumba yangu, nimeutupa urithi wangu; nimemtia mpenzi wangu katika mikono ya adui zake. 8 Urithi wangu umekuwa kwangu kama simba msituni; ameinua sauti yake juu yangu; kwa sababu hiyo nimemchukia. 9 Je! Urithi wangu umekuwa kwangu kama ndege mwenye madoadoa? Ndege wakali wanamtulia pande zote? Enendeni, wakusanyeni pamoja wanyama wote wa mwituni, waleteni ili wale. 10 Wachungaji wengi wameliharibu shamba langu la mizabibu, wamelikanyaga fungu langu chini ya miguu yao, wamefanya fungu langu zuri kuwa jangwa la ukiwa. 11 Wamelifanya kuwa ukiwa, na kwa kuwa ni ukiwa linanililia; nchi yote imefanywa kuwa ukiwa, kwa sababu hapana mtu aliyeweka haya moyoni mwake. 12 Watekao nyara wamepanda juu ya vilele vya milima katika nyika; kwa maana upanga wa Bwana utakula toka upande mmoja wa nchi hata upande wa pili wa nchi; hapana mwenye mwili atakayekuwa na amani. 13 Wamepanda ngano, lakini watavuna miiba; wamejiumiza nafsi zao, lakini hawatakuwa na faida; naam, tahayarini kwa ajili ya matunda yenu, kwa sababu ya hasira kali ya Bwana. 14 Bwana asema hivi juu ya jirani zangu wote walio wabaya, waugusao urithi wangu niliowarithisha watu wangu Israeli, Tazama, nitawang'oa katika nchi yao, nami nitaing'oa nyumba ya Yuda isiwe kati yao. 15 Tena itakuwa, baada ya kuwang'oa, nitarudi na kuwahurumia; nami nitawaleta tena, kila mtu aingie katika urithi wake, na kila mtu aingie katika nchi yake. 16 Kisha itakuwa, ikiwa watajifunza kwa bidii njia za watu wangu, kuapa kwa jina langu, Kama Bwana aishivyo, vile vile kama walivyowafundisha watu wangu kuapa kwa Baali, ndipo watakapojengwa kati ya watu wangu. 17 Bali, kama hawataki kusikia, kung'oa nitaling'oa taifa lile, na kuliangamiza kabisa, asema Bwana.

Yeremia 13

1 Bwana akaniambia hivi, Enenda, ukajinunulie mshipi wa kitani, ukajivike viuno, wala usiutie majini. 2 Basi nikanunua mshipi sawasawa na neno la Bwana, nikajivika viunoni. 3 Nalo neno la Bwana likanijia mara ya pili, kusema, 4 Twaa mshipi ule ulioununua, ulio viunoni mwako, kisha ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukaufiche huko katika pango la jabali. 5 Basi nikaenda, nikauficha karibu na mto Frati, kama Bwana alivyoniamuru. 6 Hata ikawa, baada ya siku nyingi, Bwana akaniambia, Ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukautwae ule mshipi, niliokuamuru kuuficha huko. 7 Ndipo nikaenda mpaka mto Frati, nikachimba, nikautwaa ule mshipi katika mahali pale nilipouficha; na tazama, mshipi ulikuwa umeharibika, haukufaa tena kwa lo lote. 8 Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema, 9 Bwana asema hivi, Jinsi iyo hiyo nitakiharibu kiburi cha Yuda, na kiburi kikuu cha Yerusalemu. 10 Watu hawa waovu, wanaokataa kusikiliza maneno yangu, wanaokwenda kwa ushupavu wa mioyo yao, na kufuata miungu mingine ili kuitumikia na kuiabudu, watakuwa hali moja na mshipi huu, usiofaa kwa lo lote. 11 Maana kama vile mshipi unavyoshikamana na viuno vya mtu, ndivyo nilivyowashikamanisha nami nyumba yote ya Israeli; na nyumba yote ya Yuda, asema Bwana; wapate kuwa watu kwangu mimi, na jina, na sifa, na utukufu; lakini hawakutaka kusikia. 12 Basi utawaambia neno hili, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kila chupa itajazwa divai; nao watakuambia, Je, sisi hatujui ya kuwa kila chupa itajazwa divai? 13 Ndipo utakapowaambia, Bwana asema hivi, Tazama, nitawajaza ulevi wenyeji wote wa nchi hii, hata wafalme wanaoketi katika kiti cha enzi cha Daudi, na makuhani, na manabii, na wenyeji wote wa Yerusalemu. 14 Nitawagonganisha, mtu na mwenzake, naam, baba za watu na watoto wao pamoja, asema Bwana; sitahurumia, wala sitaachilia, wala sitarehemu, hata nisiwaangamize. 15 Sikilizeni ninyi, kategeni masikio yenu; msifanye kiburi; maana Bwana amenena. 16 Mtukuzeni Bwana, Mungu wenu, kabla hajaleta giza, na kabla miguu yenu haijakwaa juu ya milima yenye giza; na wakati mnapoitazamia nuru, kabla hajaigeuza kuwa kivuli cha mauti, na giza nene. 17 Bali kama hamtaki kusikia, roho yangu italia kwa siri, kwa sababu ya kiburi chenu; na jicho langu litalia sana na kutoka machozi mengi, kwa kuwa kundi la Bwana limechukuliwa hali ya kufungwa. 18 Mwambie mfalme, na mama ya mfalme, Nyenyekeeni na kuketi chini; Kwa maana vilemba vyenu vimeshuka, naam, taji ya utukufu wenu. 19 Miji ya Negebu imefungwa malango yake, wala hapana mtu wa kuyafungua; Yuda amechukuliwa hali ya kufungwa; amechukuliwa kabisa hali ya kufungwa. 20 Inua macho yako, Ee Yerusalemu, ukawatazame hawa wanaokuja kutoka kaskazini; liko wapi kundi lako ulilopewa, kundi lile zuri? 21 Utasema nini wewe, atakapowaweka rafiki zako kuwa kichwa juu yako, ikiwa wewe mwenyewe umewafundisha kuwa juu yako? Je! Huzuni haitakushika, kama utungu wa mwanamke aliye katika kuzaa? 22 Nawe ukisema moyoni mwako, Mbona mambo haya yamenipata mimi? Ni kwa sababu ya wingi wa uovu wako, marinda yako yamefunuliwa, na visigino vya miguu yako vimeumia. 23 Je! Mkushi aweza kuibadili ngozi yake, au chui madoa-doa yake? Kama aweza, ndipo na ninyi mwaweza kutenda mema, ninyi mliozoea kutenda mabaya. 24 Kwa sababu hiyo nitawatawanya, kama makapi yapitayo, kwa upepo wa jangwani. 25 Hiyo ndiyo kura yako, fungu lako ulilopimiwa na mimi, asema Bwana; kwa kuwa umenisahau, na kuutumainia uongo. 26 Kwa ajili ya hayo, mimi nami nitayafunua marinda yako mbele ya uso wako, na aibu yako itaonekana. 27 Nimeona machukizo yako, naam, uzinifu wako, na ubembe wako, na uasherati wa ukahaba wako, juu ya milima katika mashamba. Ole wako, Ee Yerusalemu! Hutaki kutakaswa; mambo hayo yataendelea hata lini?

Yeremia 14

1 Neno la Bwana lililomjia Yeremia, katika habari ya ukosefu wa mvua. 2 Yuda huomboleza, Na malango yake yamelegea; Wameketi chini wamevaa kaniki; Na kilio cha Yerusalemu kimepaa juu. 3 Na wakuu wao huwatuma watoto wao kwenye maji; Nao hufika visimani wasione maji; Hurudi, na vyombo vyao ni vitupu; Wametahayarika na kufadhaika, Na kuvifunika vichwa vyao. 4 Kwa sababu ya nchi iliyopasuka, Kwa kuwa mvua haikunyesha katika nchi, Wenye kulima wametahayarika, Na kuvifunika vichwa vyao. 5 Naam, kulungu naye uwandani amezaa, Akamwacha mwanawe kwa kuwa hapana majani. 6 Na punda-mwitu husimama juu ya vilele vya milima, Hutwetea pumzi kama mbwa-mwitu; Macho yao hayaoni sawasawa, Kwa kuwa hapana majani. 7 Ijapokuwa maovu yetu yanatushuhudia, lakini utende wewe kwa ajili ya jina lako, Ee Bwana, maana kurudi nyuma kwetu ni kwingi; tumekutenda dhambi. 8 Wewe uliye tumaini la Israeli, wewe uliye Mwokozi wake wakati wa taabu, kwa nini wewe umekuwa kama mtu akaaye katika nchi, hali ya mgeni, na kama mtu mwenye kusafiri, ageukaye upande ili kukaa usiku mmoja tu? 9 Kwa nini wewe umekuwa kama mtu aliyesituka, kama shujaa asiyeweza kuokoa? Lakini wewe, Bwana, u katikati yetu, nasi tunaitwa kwa jina lako; usituache. 10 Bwana awaambia watu hawa hivi, Hivyo ndivyo walivyopenda kutanga-tanga; hawakuizuia miguu yao; basi, Bwana hawakubali; sasa ataukumbuka uovu wao, atawapatiliza dhambi zao. 11 Naye Bwana akaniambia, Usiwaombee watu hawa wapate heri. 12 Wafungapo, mimi sitasikia kilio chao; na watoapo sadaka za kuteketezwa na sadaka ya unga, sitazitakabali; bali nitawaangamiza kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni. 13 Ndipo nikasema, Aa, Bwana, MUNGU! Tazama, manabii huwaambia, Hamtauona upanga, wala hamtakuwa na njaa; bali nitawapa amani iliyo thabiti mahali hapa. 14 Ndipo Bwana akaniambia, Hao manabii wanatabiri uongo kwa jina langu mimi; mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao; wanawapeni unabii wa maono ya uongo, na uaguzi, na neno la ubatili, na hadaa ya mioyo yao. 15 Basi, kwa hiyo Bwana asema hivi, Kwa habari za manabii wanaotabiri kwa jina langu, wala mimi sikuwatuma, lakini husema, Upanga na njaa havitaingia katika nchi hii; Kwa upanga na njaa manabii hao wataangamizwa. 16 Na watu hao, waliopewa unabii na wao, watatupwa nje katika njia kuu za Yerusalemu kwa sababu ya upanga na njaa; wala hawatakuwa na mtu wa kuwazika, wao na wake zao, na wana wao, na binti zao; maana nitamwaga uovu wao wenyewe juu yao. 17 Nawe utawaambia neno hili, Macho yangu na yatiririke machozi, usiku na mchana, wala yasikome; kwa maana bikira, binti ya watu wangu, amevunjika mavunjiko makuu, kwa jeraha isiyoponyeka. 18 Nikitoka kwenda shambani, tazama, wako huko waliouawa kwa upanga! Na nikiingia mjini, tazama, wamo humo wanaougua kwa sababu ya njaa! Maana nabii na kuhani, wote wawili, huenda huko na huko katika nchi, wala hawana maarifa. 19 Je! Umemkataa Yuda kabisa? Roho yako imeichukia Sayuni? Mbona umetupiga, tusiwe na dawa ya kutuponya? Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote, tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu! 20 Ee Bwana, tunakiri uovu wetu, na ubaya wa baba zetu; maana tumekutenda dhambi. 21 Usituchukie, kwa ajili ya jina lako; usikifedheheshe kiti cha enzi cha utukufu wako, kumbuka, usilivunje agano ulilofanya nasi. 22 Je! Katika vitu vya ubatili vya mataifa, kiko kitu kiwezacho kuleta mvua? Je! Mbingu zaweza kutoa manyunyu? Je! Si wewe, Ee Bwana, Mungu wetu? Kwa sababu hiyo tutakungoja; kwa kuwa wewe umevifanya vitu hivi vyote.

Yeremia 15

1 Ndipo Bwana akaniambia, Hata wangesimama mbele zangu Musa na Samweli, moyo wangu usingewaelekea watu hawa; watupe, watoke mbele za macho yangu, wakaende zao. 2 Kisha itakuwa, hapo watakapokuambia, Tutoke, tuende wapi? Utawaambia, Bwana asema hivi, Walioandikiwa kufa, watakwenda kufa; au kufa kwa upanga, watakufa kwa upanga; au kufa kwa njaa, watakufa kwa njaa, au kutekwa nyara, watakuwa mateka. 3 Nami nitaamrisha juu yao namna nne, asema Bwana; upanga uue, na mbwa wararue, na ndege wa angani, na wanyama wakali wa nchi, wale na kuangamiza. 4 Nami nitawafanya kuwa kitu cha kutisha katika falme zote za duniani, kwa sababu ya Manase, mwana wa Hezekia mfalme wa Yuda, kwa sababu ya mambo aliyoyatenda katika Yerusalemu. 5 Maana ni nani atakayekuhurumia, Ee Yerusalemu? Au ni nani atakayekulilia? Au ni nani atakayegeuka upande ili kuuliza habari za hali yako? 6 Umenikataa mimi, asema Bwana, umerudi nyuma; ndiyo maana nimenyosha mkono wangu juu yako, na kukuangamiza; nimechoka kwa kughairi. 7 Nami nimewapepea kwa kipepeo katika malango ya nchi nimewaondolea watoto wao, nimewaharibu watu wangu; hata hivyo hawakurudi na kuziacha njia zao. 8 Wajane wao wameongezeka kwangu kuliko mchanga wa bahari; nimeleta mwenye kuteka wakati wa adhuhuri juu ya mama wa vijana; nimeleta hamu na maogofyo yampate ghafula. 9 Mwanamke aliyezaa watoto saba anazimia; ametoa roho; jua lake limekuchwa, ungali ni wakati wa mchana; ametahayarika na kufedheheka; na mabaki yao nitawatoa kwa upanga mbele ya adui zao, asema Bwana. 10 Ole wangu, mama yangu, kwa kuwa umenizaa mtu wa kuteta, na mtu wa kushindana na dunia yote! Mimi sikukopesha kwa riba, wala watu hawakunikopesha kwa riba; lakini kila mmoja wao hunilaani. 11 Bwana akasema, Hakika nitakutia nguvu upate mema; hakika nitamlazimisha adui akusihi wakati wa uovu, na wakati wa taabu. 12 Je! Mtu aweza kuvunja chuma, naam, chuma kitokacho kaskazini, au shaba? 13 Mali yako na hazina zako nitazitoa kuwa nyara, bila kulipwa thamani yake; naam, kwa sababu ya dhambi zako zote, hata katika mipaka yako yote. 14 Nami nitakulazimisha kuwatumikia adui zako katika nchi usiyoijua; maana moto umewashwa katika hasira yangu, utakaowateketeza ninyi. 15 Ee Bwana, unajua wewe; unikumbuke, unijilie, ukanilipie kisasi juu yao wanaoniudhi; usiniondoe kwa uvumilivu wako; ujue ya kuwa ni kwa ajili yako nilivyopatikana na mashutumu. 16 Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Bwana, Mungu wa majeshi. 17 Sikuketi katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala sikufurahi, naliketi peke yangu kwa sababu ya mkono wako; kwa maana umenijaza ghadhabu. 18 Mbona maumivu yangu ni ya daima, na jeraha yangu haina dawa, inakataa kuponywa? Je! Yamkini wewe utakuwa kwangu kama kijito kidanganyacho, na kama maji yasiyodumu? 19 Kwa sababu hiyo Bwana asema hivi, Ukirudi, ndipo mimi nitakapokurejeza, upate kusimama mbele zangu; nawe ukitoa kilicho cha thamani katika kilicho kibovu, utakuwa kama kinywa changu; nao watakurudia wewe, bali hutawarudia wao. 20 Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya, asema Bwana. 21 Nami nitakuokoa na mkono wa watu wabaya, nami nitakukomboa katika mkono wao wenye kutisha.

Yeremia 16

1 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Wewe hutaoa mke, wala hutakuwa na wana wala binti mahali hapa. 3 Maana Bwana asema hivi, katika habari za wana, na katika habari za binti, wazaliwao mahali hapa, na katika habari za mama zao waliowazaa, na katika habari za baba zao waliowazaa, katika nchi hii; 4 watakufa kwa maradhi mabaya; hawataliliwa, wala hawatazikwa; watakuwa kama samadi juu ya uso wa nchi; nao wataangamizwa kwa upanga, na kwa njaa; na mizoga yao itakuwa chakula cha ndege wa angani, na cha wanyama wa nchi. 5 Maana Bwana asema hivi, Usiingie ndani ya nyumba yenye matanga, wala usiende kuwaombolezea, wala kuwalilia; maana nimewaondolea watu hawa amani yangu, asema Bwana, hata fadhili zangu na rehema zangu. 6 Wakubwa kwa wadogo wote pia watakufa katika nchi hii; hawatazikwa, wala watu hawatawalilia, wala kujikata-kata kwa ajili yao, wala kujinyoa kwa ajili yao; 7 wala watu hawatamega mkate kwa ajili yao, wakati wa kuomboleza, ili kuwafariji kwa ajili yao waliokufa; wala watu hawatawapa kikombe cha faraja, wanywe kwa ajili ya baba yao au mama yao. 8 Wala usiingie ndani katika nyumba yenye karamu, kuketi pamoja nao, na kula na kunywa. 9 Maana Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Mimi, mbele ya macho yenu, na katika siku zenu, nitaikomesha sauti ya furaha, na sauti ya kicheko, mahali hapa; sauti ya bwana arusi, na sauti ya bibi arusi. 10 Tena itakuwa, utakapowaonyesha watu hawa maneno haya yote, nao wakakuambia, Mbona Bwana amenena juu yetu mabaya haya makuu? Uovu wetu ni uovu gani? Na dhambi yetu, tuliyomtenda Bwana, Mungu wetu, ni nini? 11 Ndipo utakapowaambia, Ni kwa sababu baba zenu wameniacha mimi, asema Bwana, na kuwafuata miungu mingine, na kuwatumikia, na kuwaabudu, wakaniacha mimi, wasiishike torati yangu; 12 na ninyi mmetenda mabaya kupita baba zenu; maana angalieni, mnaenenda kila mmoja wenu kwa ushupavu wa moyo wake mbaya, msinisikilize mimi; 13 basi, kwa sababu hiyo, nitawatoeni katika nchi hii, na kuwaingiza katika nchi ambayo hamkuijua, wala ninyi wala baba zenu; na huko mtawatumikia miungu mingine mchana na usiku; kwa maana mimi sitawapa fadhili zangu hata kidogo. 14 Kwa hiyo, angalia, siku zinakuja, asema Bwana, ambapo hawatasema tena, Aishivyo Bwana, aliyewaleta wana wa Israeli toka nchi ya Misri; 15 lakini, Aishivyo Bwana, aliyewaleta wana wa Israeli toka nchi ya kaskazini, na toka nchi zote alikowafukuza; nami nitawarudisha katika nchi yao wenyewe niliyowapa baba zao. 16 Tazama, asema Bwana, Nitatuma watu kuwaita wavuvi wengi, nao watawavua; na baada ya hayo nitatuma watu kuwaita wawindaji wengi, nao watawawinda, watoke katika kila mlima, na kila kilima, na pango za majabali. 17 Maana macho yangu yaziangalia njia zao zote, hawakufichwa uso wangu usiwaone, wala haukusitirika uovu wao macho yangu yasiuone. 18 Nami kwanza nitawalipa uovu wao na dhambi zao maradufu, kwa kuwa wameitia unajisi nchi yangu, kwa mizoga ya vitu vyao vichukizavyo, na kuujaza urithi wangu kwa machukizo yao. 19 Ee Bwana, nguvu zangu, ngome yangu, na kimbilio langu siku ya taabu, kwako wewe watakuja mataifa yote toka ncha za dunia, wakisema, Baba zenu hawakurithi kitu ila uongo, naam, ubatili na vitu visivyofaa. 20 Je! Mwanadamu ajifanyie miungu, wasio miungu? 21 Basi, tazama, nitawajulisha, mara moja hii nitawajulisha, mkono wangu, na nguvu zangu; nao watajua ya kuwa, jina langu ni YEHOVA.

Yeremia 17

1 Dhambi ya Yuda imeandikwa kwa kalamu ya chuma, na kwa ncha ya almasi; imechorwa katika kibao cha moyo wao, na katika pembe za madhabahu zenu; 2 na wakati huo watoto wao wazikumbuka madhabahu zao, na maashera yao, karibu na miti yenye majani mabichi juu ya milima mirefu. 3 Ee mlima wangu wa uwandani, nitatoa mali zako na hazina zako zote ziwe nyara, na mahali pako palipoinuka, kwa sababu ya dhambi, katika mipaka yako yote. 4 Nawe, naam, wewe nafsi yako, utaachana na urithi wako niliokupa; nami nitakulazimisha kuwatumikia adui zako katika nchi usiyoijua; maana umewasha moto katika hasira yangu, utakaowaka milele. 5 Bwana asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana. 6 Maana atakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. 7 Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni tumaini lake. 8 Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda. 9 Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? 10 Mimi, Bwana, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake. 11 Kama kware akusanyaye makinda asiyoyazaa, ndivyo alivyo mtu ajipatiaye mali, wala si kwa haki, katikati ya siku zake zitaachana naye, na mwisho wake atakuwa mpumbavu. 12 Kiti cha enzi, cha utukufu, kilichowekwa juu tangu mwanzo, ndicho mahali patakatifu petu. 13 Ee Bwana, tumaini la Israeli, wote wakuachao watatahayarika. Wao watakaojitenga nami wataandikwa katika mchanga, kwa sababu wamemwacha Bwana, kisima cha maji yaliyo hai. 14 Uniponye, Ee Bwana, nami nitaponyeka; uniokoe, nami nitaokoka; kwa maana wewe ndiwe uliye sifa zangu. 15 Tazama, wao waniambia, Neno la Bwana liko wapi? Na lije, basi. 16 Mimi hapa sikufanya haraka kuacha kuwa mchungaji nyuma yako; wala sikuitamani siku ya maradhi ya kufisha; wewe unajua; yaliyotoka midomoni mwangu yalikuwa mbele za uso wako. 17 Usiwe sababu ya hofu kuu kwangu mimi; wewe ndiwe uliye kimbilio langu siku ya uovu. 18 Na waaibike watu wanaoniudhi, lakini nisiaibike mimi; na waone hofu kuu, lakini mimi nisione hofu kuu; ulete juu yao siku ya uovu; uwaangamize maangamizo maradufu. 19 Bwana akaniambia hivi, Enenda ukasimame katika lango la wana wa watu hawa, waingiapo wafalme wa Yuda, na watokeapo, na katika malango yote ya Yerusalemu, 20 ukawaambie, Lisikieni neno la Bwana, enyi wafalme wa Yuda, na Yuda wote, nanyi wenyeji wote wa Yerusalemu, ninyi mwingiao kwa malango haya; 21 Bwana asema hivi, Jihadharini nafsi zenu, msichukue mzigo wo wote siku ya sabato, wala msiulete ndani kwa malango ya Yerusalemu; 22 wala msitoe mzigo katika nyumba zenu siku ya sabato, wala msifanye kazi yo yote; bali itakaseni siku ya sabato, kama nilivyowaamuru baba zenu; 23 lakini hawakusikiliza, wala hawakutega masikio yao, bali walifanya shingo zao kuwa ngumu, ili wasisikilize wala wasipokee mafundisho. 24 Na itakuwa, kama mkinisikiliza mimi kwa bidii, asema Bwana, msiingize mzigo wo wote kwa malango ya mji huu siku ya sabato, bali mkiitakasa siku ya sabato, bila kufanya kazi yo yote siku hiyo; 25 ndipo watakapoingia wafalme na wakuu kwa malango ya mji huu; wataketi katika kiti cha enzi cha Daudi, na kupanda magari na farasi, wao, na wakuu wao, watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu; na mji huu utakaa hata milele. 26 Nao watatoka miji ya Yuda, na mahali palipo pande zote za Yerusalemu, na nchi ya Benyamini, na Shefela, na milima,na upande wa Negebu,wakileta sadaka za kuteketezwa,na dhabihu,na sadaka za unga,na ubani,wakileta pia sadaka za shukurani,nyumbani kwa BWANA. 27 Lakini kama hamtaki kunisikiliza, kuitakasa siku ya sabato, kutokuchukua mzigo na kuingia kwa malango ya Yerusalemu siku ya sabato; basi, nitawasha moto malangoni mwake, nao utaziteketeza nyumba za enzi za Yerusalemu, wala hautazimika.

Yeremia 18

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 2 Ondoka, ukashuke mpaka nyumba ya mfinyanzi, na huko nitakusikizisha maneno yangu. 3 Basi nikashuka mpaka nyumba ya mfinyanzi, na tazama, alikuwa akifanya kazi yake kwa magurudumu. 4 Na chombo kile, alichokuwa akikifinyanga, kilipoharibika mkononi mwake yule mfinyanzi, alikifanyiza tena kuwa chombo kingine, kama alivyoona vema yule mfinyanzi kukifanya. 5 Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema, 6 Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli. 7 Wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuung'oa, na kuuvunja, na kuuangamiza; 8 ikiwa taifa lile nililolitaja litageuka, na kuacha maovu yake nitaghairi, nisitende mabaya yale niliyoazimia kuwatenda. 9 Na wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuujenga na kuupanda, 10 ikiwa watatenda maovu mbele za macho yangu, wasiitii sauti yangu, basi nitaghairi, nisitende mema yale niliyoazimia kuwatendea. 11 Haya! Basi, ukawaambie watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Tazama, ninafinyanga mabaya juu yenu, na kuwaza mawazo juu yenu; rudini sasa, kila mmoja na aiache njia yake mbaya; zitengenezeni njia zenu, na matendo yenu. 12 Lakini wao wasema, Hapana tumaini lo lote; maana sisi tutafuata mawazo yetu wenyewe, nasi tutatenda kila mmoja wetu kwa kuufuata ushupavu wa moyo wake mbaya. 13 Basi, kwa ajili ya hayo, Bwana asema hivi, Ulizeni sasa katika mataifa, ni nani aliyesikia habari za mambo kama hayo; bikira wa Israeli ametenda tendo lichukizalo sana. 14 Je! Theluji ya Lebanoni itakoma katika jabali la kondeni? Au je! Maji ya baridi yashukayo toka mbali yatakauka? 15 Maana watu wangu wamenisahau, wameufukizia ubatili uvumba; nao wamewakaza katika njia zao, katika mapito ya zamani, ili wapite katika njia za kando, katika njia isiyotengenezwa; 16 ili kufanya nchi yao kuwa kitu cha kushangaza, na cha kuzomewa daima; kila mtu apitaye karibu nayo atashangaa, na kutikisa kichwa chake. 17 Nami nitawatawanya mbele ya adui, kama kwa upepo wa mashariki; nami nitaviangalia visogo vyao, wala si nyuso zao, siku ya msiba wao. 18 Hapo ndipo waliposema, Njoni na tufanye mashauri juu ya Yeremia; maana sheria haitampotea kuhani, wala shauri halitampotea mwenye hekima, wala neno halitampotea nabii. Njoni, na tumpige kwa ndimi zetu, wala tusiyaangalie maneno yake yo yote. 19 Niangalie, Ee Bwana, ukasikilize sauti ya wanaoshindana nami. 20 Je! Mabaya yalipwe badala ya mema? Maana wameichimbia nafsi yangu shimo. Kumbuka jinsi nilivyosimama mbele zako, ili niseme mema kwa ajili yao, nikaigeuze ghadhabu yako isiwapate. 21 Kwa sababu hiyo, uwatoe watoto wao waone njaa, uwatoe nguvu za upanga ziwapate; wake zao wafiwe na watoto wao, na kufiwa na waume zao; wanaume wao wauawe, na vijana wao wapigwe kwa upanga vitani. 22 Kilio na kisikiwe kitokacho katika nyumba zao, hapo utakapoleta kikosi juu yao kwa ghafula; kwa maana wamenichimbia shimo waninase, nao wameifichia miguu yangu mitego. 23 Lakini wewe, Bwana, unajua mashauri yao yote juu yangu, ya kuniua; usiwasamehe uovu wao, wala usifute dhambi yao mbele za macho yako; bali wakwazwe mbele zako; uwatende mambo wakati wa hasira yako.

Yeremia 19

1 Bwana akasema hivi, Enenda ukanunue gudulia la mfinyanzi, ukachukue pamoja nawe baadhi ya wazee wa watu, na baadhi ya wazee wa makuhani; 2 ukatoke uende mpaka bonde la mwana wa Hinomu lililo karibu na mahali pa kuingia kwa lango la vigae, ukahubiri huko maneno nitakayokuambia, 3 ukisema, Lisikieni neno la Bwana, enyi wafalme wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu; Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli asema hivi, Angalieni, nitaleta mabaya juu ya mahali hapa, ambayo mtu ye yote akisikia habari yake, masikio yake yatawaka. 4 Kwa sababu wameniacha mimi, nao wamepafanya mahali hapa kuwa mahali pageni, nao hapa wamewafukizia uvumba miungu mingine wasiowajua, wala wao, wala baba zao, wala wafalme wa Yuda; nao wamepajaza mahali hapa damu ya wasio na hatia; 5 nao wamemjengea Baali mahali pake palipo juu, ili kuwachoma moto wana wao, wawe sadaka za kuteketezwa kwa Baali; tendo nisiloliamuru mimi, wala kulinena, wala halikuingia moyoni mwangu; 6 basi, angalieni, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo katika siku hizo mahali hapa hapataitwa tena Tofethi, wala Bonde la mwana wa Hinomu, bali, Bonde la Machinjo. 7 Nami nitalitangua shauri la Yuda na Yerusalemu mahali hapa; nami nitawaangusha kwa upanga mbele za adui zao, na kwa mkono wa watu watafutao roho zao; na mizoga yao nitawapa ndege wa angani na wanyama wakali wa nchi, iwe chakula chao. 8 Nami nitaufanya mji huu kuwa kitu cha kushangaza watu, na kuzomewa; kila mtu apitaye karibu nao atashangaa, na kuzomea kwa sababu ya mapigo yake. 9 Nami nitawalazimisha kula nyama ya wana wao, na nyama ya binti zao, nao watakula kila mmoja nyama ya rafiki yake, wakati wa mazingira na dhiki, ambayo adui zao, na watu wale watafutao roho zao, watawadhiikisha. 10 Ndipo hapo utalivunja gudulia lile, mbele ya macho ya watu wale waendao pamoja nawe, 11 na kuwaambia, Bwana wa majeshi asema hivi, Hivyo ndivyo nitakavyowavunja watu hawa, na mji huu, kama mtu avunjavyo chombo cha mfinyanzi, kisichoweza kutengenezwa tena na kuwa kizima; nao watazika watu katika Tofethi hata hapatabaki mahali pa kuzika. 12 Hivyo ndivyo nitakavyopatenda mahali hapa, asema Bwana, nao wakaao humo, hata kufanya mji huu kuwa kama Tofethi; 13 na nyumba za Yerusalemu, na nyumba za wafalme wa Yuda, zilizotiwa unajisi, zitakuwa kama mahali pa Tofethi; naam, nyumba zote ambazo juu ya dari zake wamelifukizia uvumba jeshi lote la mbinguni, na kuwamiminia miungu mingine sadaka za kunywewa. 14 Kisha Yeremia akatoka huko Tofethi, huko ambako Bwana alimtuma atoe unabii; naye akasimama katika ua wa nyumba ya Bwana, akawaambia watu wote, 15 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitaleta juu ya mji huu, na juu ya vijiji vyake vyote, mabaya yote niliyoyanena juu yake; kwa sababu wamefanya shingo zao kuwa ngumu, kusudi wasiyasikie maneno yangu.

Yeremia 20

1 Basi Pashuri, mwana wa Imeri, kuhani, aliyekuwa msimamizi mkuu katika nyumba ya Bwana, alimsikia Yeremia alipokuwa akitabiri maneno hayo. 2 Ndipo Pashuri akampiga Yeremia, nabii, akamtia katika mkatale, uliokuwa pale penye lango la juu la Benyamini, lililokuwa katika nyumba ya Bwana. 3 Hata ikawa, asubuhi, Pashuri huyo akamtoa Yeremia katika mkatale. Ndipo Yeremia akamwambia, Bwana hakukuita jina lako Pashuri, bali Magor-misabibu. 4 Maana Bwana asema hivi, Tazama, nitakufanya kuwa hofu kuu kwa nafsi yako, na kwa rafiki zako wote; nao wataanguka kwa upanga wa adui zao, na macho yako yataona hayo; nami nitatia Yuda yote katika mikono ya mfalme wa Babeli, naye atawachukua mateka mpaka Babeli, na kuwaua kwa upanga. 5 Tena mali zote za mji huu, na mapato yake yote, na vitu vyake vya thamani vyote pia, naam, hazina zote za wafalme wa Yuda, nitavitia katika mikono ya adui zao, watakaowateka nyara, na kuwakamata, na kuwachukua mpaka Babeli. 6 Na wewe, Pashuri, na watu wote wanaokaa katika nyumba yako, mtakwenda utumwani; nawe utafika Babeli, na huko utakufa, na huko utazikwa, wewe, na rafiki zako wote, uliowatabiria maneno ya uongo. 7 Ee Bwana, umenihadaa, nami nimehadaika; wewe una nguvu kuliko mimi, ukashinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha, mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki. 8 Maana kila ninenapo napiga kelele, nalia, Dhuluma na uharibifu! Kwa kuwa neno la Bwana limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. 9 Nami nikisema, Sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake; basi, ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia. 10 Maana nimesikia mashutumu ya watu wengi; hofu ziko pande zote. Rafiki zangu wote, wanaonivizia nisite, husema, Mshitaki, nasi tutamshitaki, huenda akahadaika, nasi tutamshinda, tutajilipiza kisasi kwake. 11 Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe. 12 Lakini, Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu. 13 Mwimbieni Bwana; msifuni Bwana; Kwa maana ameiponya roho ya mhitaji Katika mikono ya watu watendao maovu. 14 Na ilaaniwe siku niliyozaliwa, isibarikiwe siku ile aliyonizaa mama yangu. 15 Na alaaniwe mtu yule aliyemletea baba yangu habari, akisema, Umezaliwa mtoto mwanamume; akimfurahisha. 16 Mtu huyo na awe kama miji ile, ambayo Bwana aliiangamiza, asijute; na asikie kilio asubuhi, na kelele za fujo adhuhuri; 17 kwa sababu hakuniua nilipotoka tumboni, na hivyo mama yangu angekuwa kaburi langu, na mimba yake sikuzote nzito. 18 Nalitoka tumboni kwa sababu gani, kuona taabu na huzuni, hata siku zangu ziharibike katika aibu?

Yeremia 21

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, hapo mfalme Sedekia alipompelekea Pashuri, mwana wa Malkiya, na Sefania, mwana wa Maaseya, kuhani, kusema, 2 Tafadhali utuulizie habari kwa Bwana; kwa maana Nebukadreza, mfalme wa Babeli, analeta vita juu yetu; labda Bwana atatutendea sawasawa na kazi zake zote za ajabu, ili aende zake akatuache. 3 Basi Yeremia akawaambia, Mwambieni Sedekia neno hili, 4 Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Angalieni, nitazigeuza nyuma silaha za vita zilizo mikononi mwenu, ambazo kwa hizo ninyi mnapigana na mfalme wa Babeli, na Wakaldayo, wanaowahusuru nje ya kuta zenu, nami nitazikusanya pamoja katikati ya mji huu. 5 Na mimi mwenyewe nitapigana nanyi, kwa mkono ulionyoshwa na kwa mkono hodari, naam, kwa hasira, na kwa ukali, na kwa ghadhabu nyingi. 6 Nami nitawapiga wenyeji wa mji huu, wanadamu na wanyama pia; watakufa kwa tauni kubwa. 7 Na baada ya hayo, asema Bwana, nitamtia Sedekia, mfalme wa Yuda, na watumishi wake, na watu wote waliosalia ndani ya mji huu, baada ya tauni ile, na upanga, na njaa, katika mkono wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao; naye atawaua kwa ukali wa upanga; hatawaachilia, wala hatawahurumia, wala hatawarehemu. 8 Nawe waambie watu hawa, Bwana asema hivi, Tazama naweka mbele yenu njia ya uzima, na njia ya mauti. 9 Yeye atakayekaa katika mji huu atakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; bali yeye atakayetoka, na kujitia pamoja na Wakaldayo wanaowahusuru, yeye ataishi, na maisha yake yatakuwa nyara kwake. 10 Maana nimeweka uso wangu juu ya mji huu niuletee mabaya, wala nisiuletee mema, asema Bwana; utatiwa katika mkono wa mfalme wa Babeli, naye atauteketeza. 11 Na katika habari za nyumba ya mfalme wa Yuda, lisikieni neno la Bwana, 12 Ee nyumba ya Daudi, Bwana asema hivi, Hukumuni hukumu ya haki asubuhi, mkawaponye waliotekwa nyara na mkono wake aliyewadhulumu, ghadhabu yangu isije ikatoka kama moto, ikaunguza, asiweze mtu ye yote kuuzima, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu. 13 Tazama, mimi ni juu yako, Ewe ukaaye bondeni, na kwenye jabali la uwandani, asema Bwana ninyi mnaosema, Ni nani atakayeshuka apigane nasi? Au, Ni nani atakayeingia katika makao yetu? 14 Nami nitawaadhibu kwa kadiri ya matunda ya matendo yenu, asema Bwana; nami nitawasha moto katika msitu wake, nao utateketeza vitu vyote viuzungukavyo.

Yeremia 22

1 Bwana akasema hivi, Shuka nyumbani kwa mfalme wa Yuda, ukaseme neno hili huko, 2 ya kwamba, Sikia neno la Bwana, Ee mfalme wa Yuda; wewe uketiye katika kiti cha enzi cha Daudi, wewe, na watumishi wako, na watu wako wote waingiao kwa malango haya; 3 Bwana asema hivi, Fanyeni hukumu na haki, mkamtoe yeye aliyetekwa katika mikono ya mdhalimu; wala msiwatende mabaya mgeni, wala yatima, wala mjane, wala kuwadhulumu, wala msimwage damu ya mtu asiye na hatia katika mahali hapa. 4 Kwa maana mkifanya haya kweli kweli, ndipo watakapoingia kwa malango ya nyumba hii wafalme wenye kuketi katika kiti cha enzi cha Daudi, wanakwenda kwa magari, na wamepanda farasi yeye, na watumishi wake, na watu wake. 5 Lakini kama hamtaki kusikia maneno haya, mimi naapa kwa nafsi yangu, asema Bwana, ya kuwa nyumba hii itakuwa ukiwa. 6 Kwa maana Bwana asema hivi, katika habari ya nyumba ya mfalme wa Yuda; Wewe u Gileadi kwangu, na kichwa cha Lebanoni; Ila hakika nitakufanya kuwa jangwa, na miji isiyokaliwa na watu. 7 Nami nitakufanyia tayari watu wenye kuharibu, kila mtu na silaha zake; Nao watakata mierezi miteule yako, na kuitupa motoni. 8 Na mataifa mengi watapita karibu na mji huu, nao watasema kila mtu na jirani yake, Nini maana yake Bwana kuutenda hivi mji huu mkubwa? 9 Ndipo watakapojibu, Ni kwa sababu waliliacha agano la Bwana, Mungu wao, wakaabudu miungu mingine, na kuitumikia. 10 Msimlilie aliyekufa, wala msimwombolezee, Bali mlilieni huyo aendaye zake mbali; Kwa maana yeye hatarudi tena, Wala hataiona nchi aliyozaliwa. 11 Maana Bwana asema hivi, katika habari za Shalumu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda; aliyemiliki badala ya Yosia, baba yake, yeye aliyetoka mahali hapa; Hatarudi huku tena; 12 bali katika mahali pale walipomchukua mateka ndipo atakapokufa, wala hataiona nchi hii tena kamwe. 13 Ole wake aijengaye nyumba yake kwa uovu! Na vyumba vyake kwa udhalimu! Atumiaye utumishi wa mwenzake bila ujira, Wala hampi mshahara wake; 14 Asemaye, Nitajijengea nyumba pana na vyumba vipana; Naye hujikatia madirisha; Na kuta zake zimefunikwa kwa mierezi, Na kupakwa rangi nyekundu. 15 Je! Utatawala kwa sababu unashindana na watu kwa mierezi? Baba yako, je! Hakula na kunywa, na kufanya hukumu na haki? Hapo ndipo alipofanikiwa. 16 Alihukumu maneno ya maskini na mhitaji; hapo ndipo alipofanikiwa. Je! Huku siko kunijua, asema Bwana? 17 Bali macho yako na moyo wako hauna utakalo ila kutamani, na kumwaga damu isiyo na hatia, na kudhulumu, na kutenda jeuri. 18 Basi, Bwana asema hivi, katika habari ya Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda; Hawatamwombolezea, wakisema, Aa! Ndugu yangu; au, Aa! Dada yangu; wala hawatamlilia, wakisema, Aa! Bwana wangu; au, Aa! Utukufu wake. 19 Atazikwa maziko ya punda, akibururwa, na kutupwa nje ya malango ya Yerusalemu. 20 Haya panda Lebanoni, ukalie Upalize sauti yako katika Bashani; Ukalie kutoka Abarimu; Maana wapenzi wako wote wameangamia. 21 Mimi nalisema nawe wakati wa kufanikiwa kwako; lakini ulisema, Sitaki kusikia. Hii ndiyo iliyokuwa desturi yako tangu ujana wako, kutokuitii sauti yangu. 22 Upepo utawalisha wachungaji wako wote, na wapenzi wako watakwenda kufungwa; hakika wakati huo utatahayarika, na kufadhaika kwa sababu ya uovu wako wote. 23 Wewe ukaaye Lebanoni, Ufanyaye kioto chako katika mierezi, Utakuwa na hali ya kuhurumiwa sana, Upatapo utungu kama wa mwanamke azaaye. 24 Kama niishivyo mimi, asema Bwana, hata Konia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, angekuwa pete yenye muhuri katika mkono wangu wa kuume, ningekung'oa wewe hapo; 25 nami nitakutia katika mikono ya watu wale wakutafutao roho yako, na katika mikono yao unaowaogopa, naam, katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na katika mikono ya Wakaldayo. 26 Nami nitakutupa nje, wewe na mama yako aliyekuzaa, mwende nchi nyingine ambayo hamkuzaliwa huko, nanyi mtakufa huko. 27 Lakini nchi ile ambayo wanatamani kuirudia, hawatairudia kamwe. 28 Je! Mtu huyu, Konia, ni chombo kilichodharauliwa, na kuvunjika? Ni chombo kisichopendeza? Mbona wametupwa, yeye na wazao wake, na kutupwa katika nchi wasiyoijua? 29 Ee nchi, nchi, nchi, lisikie neno la Bwana. 30 Bwana asema hivi, Andikeni habari za mtu huyu kwamba hana watoto, kwamba mtu huyu hatafanikiwa siku zake zote; maana hapana mtu katika wazao wake atakayefanikiwa, akiketi katika kiti cha enzi cha Daudi, na kutawala tena katika Yuda.

Yeremia 23

1 Ole wao wachungaji, wanaoharibu kondoo za malisho yangu na kuwatawanya! Asema Bwana. 2 Kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, juu ya wachungaji wanaowalisha watu wangu, Mmetawanya kundi langu, na kuwafukuza, wala hamkwenda kuwatazama; angalieni, nitawapatiliza uovu wa matendo yenu, asema Bwana. 3 Nami nitakusanya mabaki ya kundi langu, katika nchi zile zote nilizowafukuza, nami nitawaleta tena mazizini mwao; nao watazaa na kuongezeka. 4 Nami nitaweka juu yao wachungaji watakaowalisha; wala hawataona hofu tena, wala kufadhaika, wala hatapotea hata mmoja wao, asema Bwana. 5 Tazama siku zinakuja, asema Bwana, nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi. 6 Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu. 7 Kwa hiyo, angalia, siku zinakuja, asema Bwana, ambapo hawatasema tena, Aishivyo Bwana, aliyewatoa wana wa Israeli katika nchi ya Misri; 8 lakini, Aishivyo Bwana, aliyewapandisha na kuwaongoza wazao wa nyumba ya Israeli kutoka nchi ya kaskazini, na kutoka nchi zote nilikowafukuza; nao watakaa katika nchi yao wenyewe. 9 Katika habari za manabii. Moyo wangu ndani yangu umevunjika, Mifupa yangu yote inatikisika. Nimekuwa kama mtu aliye mlevi, Na kama mtu aliyeshindwa na divai;kwa ajili ya Bwana,na kwa ajili ya maneno yake matakatifu. 10 Maana nchi imejaa wazinzi; kwa sababu ya kuapa nchi inaomboleza; malisho ya nyikani yamekauka; mwenendo wao ni mbaya, na nguvu zao si za haki. 11 Maana nabii, na kuhani, wote wawili wanakufuru; naam, katika nyumba yangu nimeuona uovu wao, asema Bwana. 12 Kwa ajili ya hayo njia yao itakuwa kwao kama mahali pa kuteleza gizani; watatelemshwa na kuanguka hapo; kwa maana nitaleta uovu juu yao, naam, mwaka wa kujiliwa kwao, asema Bwana. 13 Nami nimeona upumbavu katika manabii wa Samaria; walitabiri kwa Baali, wakawakosesha watu wangu Israeli. 14 Katika manabii wa Yerusalemu nimeona neno linalochukiza sana; hufanya zinaa; huenenda katika maneno ya uongo, hutia nguvu mikono ya watendao maovu, hata ikawa hapana mtu arejeaye na kuuacha uovu wake; wote pia wamekuwa kama Sodoma kwangu, na wenyeji wake kama Gomora. 15 Basi Bwana wa majeshi asema hivi, katika habari ya manabii, Tazama, nitawalisha pakanga, nitawanywesha maji ya uchungu; kwa kuwa kutoka kwa manabii hao wa Yerusalemu kukufuru kumeingia katika nchi yote. 16 Bwana wa majeshi asema hivi, Msisikilize maneno ya manabii wakiwatabiria; huwafundisha ubatili; hunena maono ya mioyo yao wenyewe; hayakutoka katika kinywa cha Bwana. 17 Daima huwaambia wao wanaonidharau, Bwana amesema, Mtakuwa na amani; nao humwambia kila mtu aendaye kwa ukaidi wa moyo wake, Hamtapatwa na ubaya wo wote. 18 Maana, ni nani aliyesimama katika baraza la Bwana, hata akalifahamu neno lake na kulisikia? Ni nani aliyelitia moyoni neno langu, na kulisikia? 19 Tazama, tufani ya Bwana, yaani, ghadhabu yake, imetokea; ni dhoruba ya kisulisuli; itapasuka, na kuwaangukia waovu vichwani. 20 Hasira ya Bwana haitarudi, hata atakapokwisha kuyatimiza makusudi ya moyo wake; katika siku za mwisho mtalifahamu neno hili kabisa. 21 Mimi sikuwatuma manabii hao, lakini walikwenda mbio; sikusema nao, lakini walitabiri. 22 Lakini kama wangalisimama katika baraza yangu, ndipo wangaliwasikizisha watu wangu maneno yangu, na kuwageuza waziache njia zao mbaya, na uovu wa matendo yao. 23 Mimi ni Mungu aliye karibu, asema Bwana, mimi si Mungu aliye mbali. 24 Je, mtu ye yote aweza kujificha mahali pa siri, nisimwone? Asema Bwana. Je! Mbingu na nchi hazikujawa nami? Asema Bwana. 25 Nimesikia waliyoyasema manabii wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema, Nimeota ndoto; nimeota ndoto. 26 Je! Mambo hayo yatakuwa katika mioyo ya manabii wanaotabiri uongo hata lini, manabii hao wenye udanganyifu katika mioyo yao wenyewe? 27 Wanaodhania ya kuwa watawasahaulisha watu wangu jina langu kwa ndoto zao, wanazomhadithia kila mtu jirani yake, kama vile baba zao walivyolisahau jina langu, kwa ajili ya Baali. 28 Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. 29 Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande? 30 Basi kwa sababu hiyo mimi ni juu ya manabii hao, asema Bwana, wanaompokonya kila mtu jirani yake maneno yangu. 31 Tazama, mimi ni juu ya manabii, asema Bwana, wanaotumia ndimi zao na kusema, Yeye asema, 32 Tazama, mimi ni juu ya hao wanaotabiri ndoto za uongo, asema Bwana, na kuzisema, na kuwakosesha watu wangu kwa uongo wao, na kwa majivuno yao ya upuzi, lakini mimi sikuwatuma, wala sikuwapa amri; wala hawatawafaidia watu hawa hata kidogo, asema Bwana. 33 Na watu hawa, au nabii au kuhani, atakapokuuliza, akisema, Mzigo wa Bwana ni nini? Ndipo utawaambia, Mzigo gani? Bwana asema, Nitawatupilia mbali. 34 Na katika habari ya nabii, na kuhani, na watu, watakaosema, Mzigo wa Bwana, mimi nitamwadhibu mtu yule, na nyumba yake. 35 Mtasema hivi kila mtu na jirani yake, na kila mtu na ndugu yake, Bwana amejibu mtu? Na, Bwana amesemaje? 36 Na mzigo wa Bwana hamtautaja tena; maana neno la kila mtu ndilo litakalokuwa mzigo wake; maana ninyi mmeyapotosha maneno ya Mungu aliye hai, ya Bwana wa majeshi, Mungu wetu. 37 Nawe utamwambia nabii hivi, Bwana amekujibu nini? Na, Bwana amesemaje? 38 Lakini mkisema, Mzigo wa Bwana, basi, Bwana asema hivi, Kwa sababu mwasema neno hili, ; nami nimemtuma mtu kwenu kusema, Msiseme, ; 39 basi, kwa hiyo angalieni, nitawasahau ninyi kabisa, nami nitawatupilia mbali, pamoja na mji huu niliowapa ninyi na baba zenu, mtoke mbele za uso wangu; 40 nami nitaleta juu yenu aibu ya milele, na fedheha ya daima, ambayo haitasahauliwa.

Yeremia 24

1 Bwana akanionyesha, na tazama, vikapu viwili vya tini, vimewekwa mbele ya hekalu la Bwana, baada ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, kumchukua mateka Yekonia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, na wakuu wa Yuda, pamoja na mafundi na wafua chuma, kutoka Yerusalemu, kuwaleta Babeli. 2 Kikapu kimoja kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini zilizotangulia kuiva; na kikapu cha pili kilikuwa na tini mbovu sana zisizoweza kuliwa, kwa kuwa zilikuwa mbovu sana. 3 Ndipo Bwana akaniambia, Unaona nini Yeremia? Nikasema, Naona tini; tini nzuri zilizo nzuri sana; na tini mbovu zilizo mbovu sana, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu sana. 4 Kisha neno la Bwana likanijia, kusema, 5 Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kama zilivyo tini hizi nzuri, ndivyo nitakavyowaangalia mateka wa Yuda, niliowatoa katika mahali hapa, waende mpaka nchi ya Wakaldayo, wapate mema. 6 Kwa maana nitawatulizia macho yangu, wapate mema, nami nitawaingiza katika nchi hii tena; nami nitawajenga, wala sitawabomoa; nitawapanda wala sitawang'oa. 7 Nami nitawapa moyo, wanijue ya kuwa mimi ni Bwana; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; kwa maana watanirudia kwa moyo wao wote. 8 Na habari za tini zile mbovu, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu sana; hakika, asema, Bwana, ndivyo nitakavyomtoa Sedekia, mfalme wa Yuda, na wakuu wake, na mabaki ya Yerusalemu, waliosalia katika nchi hii, na hao wanaokaa katika nchi ya Misri. 9 Naam, nitawatoa watupwe huko na huko katika falme zote za dunia, wapate mabaya; wawe kitu cha kulaumiwa, na mithali, na dhihaka, na laana, katika mahali pote nitakapowafukuza. 10 Nami nitatuma upanga, na njaa, na tauni, kati yao, hata watakapopotelea mbali katika nchi niliyowapa, wao na baba zao.

Yeremia 25

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, katika habari za watu wote wa Yuda; katika mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda mwaka ule ndio mwaka wa kwanza wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli; 2 ambalo Yeremia, nabii, aliwaambia watu wote wa Yuda, na wenyeji wote wa Yerusalemu, kusema, 3 Tangu mwaka wa kumi na tatu wa kutawala kwake Yosia, mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda, hata siku hii ya leo, miaka hii ishirini na mitatu, neno la Bwana limenijia, nami nimesema nanyi, nikiamka mapema na kusema; lakini ninyi hamkusikiliza. 4 Naye Bwana ametuma kwenu watumishi wake wote, hao manabii, akiamka mapema na kuwatuma, lakini ninyi hamkusikiliza, wala hamkutega masikio yenu, msikilize. 5 Akasema, Rudini sasa, kila mtu na aiache njia yake mbaya; uacheni uovu wa matendo yenu, mkae katika nchi ambayo Bwana aliwapa, ninyi na baba zenu, tangu zamani za kale na hata milele; 6 wala msiwafuate miungu mingine, ili kuwatumikia na kuwasujudia, wala msinikasirishe kwa kazi ya mikono yenu; basi, mimi sitawadhuru ninyi kwa dhara lo lote. 7 Lakini ninyi hamkunisikiliza, asema Bwana; ili mnikasirishe kwa kazi ya mikono yenu, na kujidhuru nafsi zenu. 8 Basi Bwana wa majeshi asema hivi, Kwa kuwa hamkuyasikiliza maneno yangu, 9 angalieni, nitapeleka watu na kuzitwaa jamaa zote za upande wa kaskazini, asema Bwana, nami nitatuma ujumbe kwa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mtumishi wangu, nami nitawaleta juu ya nchi hii, na juu yao wakaao ndani yake, na juu ya mataifa haya yote yaliyopo pande zote; nami nitawaangamiza kabisa, na kuwafanya kitu cha kushangaza, na kitu cha kuzomewa, na ukiwa wa daima. 10 Tena, nitawaondolea sauti ya kicheko, na sauti ya furaha, sauti ya bwana arusi, na sauti ya bibi arusi, sauti ya mawe ya kusagia, na nuru ya mishumaa. 11 Na nchi hii yote pia itakuwa ukiwa, na kitu cha kushangaza; nayo mataifa haya watamtumikia mfalme wa Babeli miaka sabini. 12 Na itakuwa miaka hiyo sabini itakapotimia, nitamwadhibu mfalme wa Babeli, na taifa lile, asema Bwana, kwa sababu ya uovu wao, nayo nchi ya Wakaldayo pia; nami nitaifanya kuwa ukiwa wa milele. 13 Nami nitaleta juu ya nchi ile maneno yangu yote niliyoyanena juu yake, naam, yote yaliyoandikwa ndani ya kitabu hiki, aliyotabiri Yeremia juu ya mataifa haya yote. 14 Kwa maana mataifa mengi na wafalme wakuu watawatumikisha; naam, hao pia; nami nitawalipa kwa kadiri ya matendo yao, na kwa kadiri ya kazi ya mikono yao. 15 Maana Bwana, Mungu wa Israeli, aniambia hivi, Pokea kikombe cha divai ya ghadhabu hii mkononi mwangu, ukawanyweshe mataifa yote, ambao nitakupeleka kwao; 16 nao watakunywa, na kulewalewa, na kufanya wazimu, kwa sababu ya upanga nitakaoupeleka kati yao. 17 Ndipo nikakipokea kikombe kile mkononi mwa Bwana, nikawanywesha mataifa yote, ambao Bwana alinipeleka kwao; 18 yaani, Yerusalemu, na miji ya Yuda, na wafalme wake, na wakuu wake, ili kuwafanya kuwa ukiwa, na ajabu, na mazomeo, na laana; vile vile kama ilivyo leo; 19 Farao, mfalme wa Misri, na watumishi wake na wakuu wake na watu wake wote; 20 na watu wote waliochanganyika pamoja, na wafalme wote wa nchi ya Uzi, na wafalme wote wa nchi ya Wafilisti, na Ashkeloni, na Gaza, na Ekroni, na mabaki ya Ashdodi; 21 Edomu, na Moabu, na wana wa Amoni; 22 na wafalme wote wa Tiro, na wafalme wote wa Sidoni, na wafalme wote wa kisiwa kilicho ng'ambo ya pili ya bahari; 23 Dedani, na Tema, na Buzi, na watu wote wakatao denge; 24 na wafalme wote wa Arabuni, na wafalme wote wa watu waliochanganyika wakaao jangwani; 25 na wafalme wote wa Zimri, na wafalme wote wa Elamu, na wafalme wote wa Wamedi; 26 na wafalme wote wa kaskazini, walio mbali na walio karibu, wote pamoja; na wafalme wote wa dunia, wakaao juu ya uso wa dunia; na mfalme wa Sheshaki atakunywa baada yao. 27 Nawe utawaambia hivi, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nyweni, na kulewa, na kutapika, na kuanguka msiinuke tena, kwa sababu ya upanga nitakaoupeleka kati yenu. 28 Tena itakuwa, kama wakikataa kukipokea kikombe kile mkononi mwako, wanywe, ndipo utakapowaambia, Bwana wa majeshi asema hivi, Lazima mtakunywa. 29 Maana angalieni, ninaanza kutenda mabaya katika mji uitwao kwa jina langu, je! Mtaachiliwa ninyi msiadhibiwe? Hamtaachiliwa msiadhibiwe; kwa maana nitauita upanga ule uwapige wote wakaao katika dunia, asema Bwana wa majeshi. 30 Basi, tabiri wewe maneno haya yote juu yao, na kuwaambia, Bwana atanguruma toka juu, Naye atatoa sauti yake toka patakatifu pake; Atanguruma sana juu ya zizi lake; Atapiga kelele kama mtu akanyagaye zabibu, Juu ya wenyeji wote wa dunia. 31 Mshindo utafika hata mwisho wa dunia; Maana Bwana ana mashindano na mataifa, Atateta na watu wote wenye mwili; Na waovu atawatoa wauawe kwa upanga; asema Bwana. 32 Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama, uovu utatokea toka taifa hata taifa, na tufani kuu itainuliwa toka pande za mwisho wa dunia. 33 Na waliouawa na Bwana siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi. 34 Pigeni yowe, enyi wachungaji, na kulia; na kugaagaa katika majivu, enyi mlio hodari katika kundi; maana siku za kuuawa kwenu zimetimia kabisa, nami nitawavunja vipande vipande, nanyi mtaanguka kama chombo cha anasa. 35 Nao wachungaji watakuwa hawana njia ya kukimbia, wala walio hodari katika kundi hawataokoka. 36 Sauti ya kilio cha wachungaji, na sauti ya kupiga yowe kwao walio hodari katika kundi, kwa maana Bwana anayaharibu malisho yao. 37 Na mazizi yenye amani yamenyamazishwa, kwa sababu ya hasira kali ya Bwana. 38 Ameacha mahali pake pa kujificha, kama simba; maana nchi yao imekuwa kitu cha kushangaza, kwa sababu ya ukali wa upanga uoneao, na kwa sababu ya hasira yake kali.

Yeremia 26

1 Mwanzo wa kumiliki kwake Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilitoka kwa Bwana, kusema, 2 Bwana asema hivi, Simama katika uwanja wa nyumba ya Bwana, useme na miji yote ya Yuda, wajao ili kuabudu katika nyumba ya Bwana; sema nao maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja. 3 Labda watasikia, na kughairi na kuacha kila mtu njia yake mbaya; ili niyaghairi mabaya niliyokusudia kuwatenda, kwa sababu ya uovu wa matendo yao. 4 Nawe utawaambia, Bwana asema hivi, Kama hamtaki kunisikia, kwenda katika sheria yangu, niliyoiweka mbele yenu, 5 kuyasikiliza maneno ya watumishi wangu, manabii, ninaowatuma kwenu, naam, nikiondoka mapema na kuwatuma; lakini ninyi hamkuwasikiliza; 6 basi, nitafanya nyumba hii kuwa kama Shilo, na mji huu nitaufanya kuwa laana kwa taifa zote za dunia. 7 Na makuhani, na manabii, na watu wote, wakamsikia Yeremia, hapo aliposema maneno haya katika nyumba ya Bwana. 8 Ikawa, Yeremia alipokuwa amekwisha kusema maneno yote Bwana aliyomwamuru kuwaambia watu wote, ndipo hao makuhani, na manabii, na watu wote, wakamkamata, wakisema, Bila shaka utakufa. 9 Kwa nini umetabiri kwa jina la Bwana, ukisema, Nyumba hii itakuwa kama Shilo, na mji huu utakuwa ukiwa, hautakaliwa na mtu? Watu wote wakamkusanyikia Yeremia katika nyumba ya Bwana. 10 Na wakuu wa Yuda waliposikia habari za mambo haya, wakatoka katika nyumba ya mfalme, wakapanda juu mpaka nyumbani kwa Bwana; wakaketi, hapo watu waingiapo katika lango jipya la nyumba ya Bwana. 11 Ndipo hapo makuhani, na manabii, wakawaambia wakuu na watu wote, wakisema, Mtu huyu amestahili kufa, kwa sababu ametabiri juu ya mji huu, kama mlivyosikia kwa masikio yenu. 12 Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote, akisema, Bwana ndiye aliyenituma kutabiri juu ya nyumba hii, na juu ya mji huu, maneno hayo yote mliyoyasikia. 13 Basi sasa, tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, mkaisikilize sauti ya Bwana, Mungu wenu; naye Bwana atayaghairi mabaya aliyoyanena juu yenu. 14 Lakini kwangu mimi, tazama, mimi nipo hapa mikononi mwenu; nitendeni myaonayo kuwa mema na haki mbele ya macho yenu. 15 Lakini jueni yakini ya kuwa, mkiniua, mtajiletea juu yenu damu isiyo na hatia itakuwa juu yenu, na juu ya mji huu, na juu ya wenyeji wake; kwa maana ni kweli Bwana amenituma kwenu, kuwaambieni yote mliyoyasikia. 16 Ndipo wakuu na watu wote wakawaambia makuhani, na manabii, wakisema, Mtu huyu hastahili kuuawa; kwa maana amesema nasi katika jina la Bwana Mungu wetu. 17 Ndipo watu kadha wa kadha miongoni mwa wazee wa nchi wakaondoka, wakanena na mkutano wa watu, wakisema, 18 Mikaya Mmorashti, alitabiri katika siku za Hezekia, mfalme wa Yuda; akasema na watu wote wa Yuda, ya kwamba, Bwana wa majeshi asema hivi, Sayuni utalimwa kama shamba lilimwavyo, na Yerusalemu utakuwa magofu, na mlima wa nyumba utakuwa kama mahali palipoinuka msituni. 19 Je! Hezekia, mfalme wa Yuda, na watu wote wa Yuda, walimwua Mikaya? Je! Hakumcha Bwana, na kumwomba Bwana awafadhili; naye Bwana akaghairi, asiyatende mabaya yale aliyoyatamka juu yao? Na sisi tungetenda mabaya makuu juu ya roho zetu. 20 Tena, kulikuwa na mtu aliyetabiri katika jina la Bwana, Uria, mwana wa Shemaya, wa Kiriath-Yearimu; yeye naye alitabiri juu ya mji huu, na juu ya nchi hii, sawasawa na maneno yote ya Yeremia; 21 na Yehoyakimu, mfalme, na mashujaa wake wote, na wakuu wake wote, waliposikia maneno yake, mfalme akataka kumwua; lakini Uria alipopata habari, aliogopa, akakimbia akaenda Misri. 22 Basi, mfalme Yehoyakimu akatuma watu waende Misri, Elnathani, mwana wa Akbori, na watu wengine pamoja naye, kwenda Misri; 23 wakamtoa Uria katika Misri, wakamleta kwa Yehoyakimu, mfalme; naye akamwua kwa upanga, akamtupa yule maiti katika makaburi ya watu wasio na cheo. 24 Lakini mkono wa Ahikamu, mwana wa Shafani, alikuwa pamoja na Yeremia, wasimtie katika mikono ya watu auawe.

Yeremia 27

1 Mwanzo wa kumiliki kwake Sedekia, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili likamjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 2 Bwana ameniambia hivi, Jifanyizie vifungo na nira, ukajivike shingoni; 3 kisha uvipeleke kwa mfalme wa Edomu, na mfalme wa Moabu, na mfalme wa wana wa Amoni, na mfalme wa Tiro, na mfalme wa Sidoni, kwa mikono ya wajumbe watakaofika Yerusalemu kwa Sedekia, mfalme wa Yuda. 4 Uwaagize waende kwa bwana zao, na kuwaambia, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Mtawaambia bwana zenu maneno haya; 5 Mimi nimeiumba dunia hii, wanadamu na wanyama walio juu ya uso wa nchi, kwa uweza wangu mkuu, na kwa mkono wangu ulionyoshwa; nami nawapa watu kama inipendezavyo. 6 Na sasa nimetia nchi hizi zote katika mkono wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mtumishi wangu; na wanyama wa mwituni pia nimempa wamtumikie. 7 Na mataifa yote watamtumikia yeye, na mwanawe, na mwana wa mwanawe, hata utakapowadia wakati wa nchi yake mwenyewe, ndipo mataifa mengi na wafalme wakuu watamtumikisha yeye. 8 Na itakuwa, taifa lile na mfalme yule asiyetaka kumtumikia Nebukadreza, huyo mfalme wa Babeli, na kutia shingo zao katika nira ya mfalme wa Babeli, mimi nitaliadhibu taifa lile kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni, asema Bwana, hata nitakapokuwa nimewaangamiza kwa mkono wake. 9 Lakini, katika habari zenu, msisikilize manabii wenu, wala wabashiri wenu, wala ndoto zenu, wala watambuzi wenu, wala waganga wenu, wanaowaambia, ya kwamba, Hamtamtumikia mfalme wa Babeli; 10 maana wanawatabiria uongo, ili kuwatoa ninyi mbali na nchi yenu; niwafukuze mkaangamie. 11 Bali taifa lile watakaotia shingo zao katika nira ya mfalme wa Babeli, na kumtumikia, taifa hilo nitawaacha wakae katika nchi yao wenyewe, asema Bwana; nao watailima, na kukaa ndani yake. 12 Nikamwambia Sedekia, mfalme wa Yuda, kwa mfano wa maneno hayo yote, nikisema, Tieni shingo zenu katika nira ya mfalme wa Babeli, mkamtumikie yeye na watu wake, mpate kuishi. 13 Mbona mnataka kufa, wewe na watu wako, kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni, kama Bwana alivyosema katika habari ya taifa lile, lisilotaka kumtumikia mfalme wa Babeli? 14 Wala msisikilize maneno ya manabii wawaambiao ninyi, ya kwamba, Hamtamtumikia mfalme wa Babeli; maana wanawatabiria uongo. 15 Kwa maana mimi sikuwatuma, asema Bwana, bali wanatabiri uongo kwa jina langu; nipate kuwatoeni nje, mkaangamie, ninyi, na manabii hao wanaowatabiria. 16 Pia nalisema na makuhani, na watu wote, nikisema, Bwana asema hivi, Msisikilize maneno ya manabii wenu, wanaowatabiria, wakisema, Tazameni, vyombo vya nyumba ya Bwana, baada ya muda kidogo, vitaletwa tena toka Babeli; maana wanawatabiria uongo. 17 Msiwasikilize; mtumikieni mfalme wa Babeli, mkaishi; kwani mji huu kufanywa ukiwa? 18 Lakini ikiwa hao ni manabii, na ikiwa neno la Bwana liko kwao, basi na wamwombe Bwana wa majeshi, kwamba vyombo vile vilivyosalia katika nyumba ya Bwana, na katika nyumba ya mfalme wa Yuda, na hapa Yerusalemu, visiende Babeli. 19 Maana Bwana wa majeshi asema hivi, katika habari za nguzo, na katika habari za bahari, na katika habari za matako yake, na katika habari za mabaki ya vyombo vilivyoachwa katika mji huu, 20 ambavyo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, hakuvichukua, hapo alipomchukua Yekonia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, toka Yerusalemu mpaka Babeli, pamoja na wakuu wote wa Yuda, na Yerusalemu; 21 naam, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, katika habari za vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Bwana, na katika nyumba ya mfalme wa Yuda, na hapa Yerusalemu; 22 Vitachukuliwa mpaka Babeli, navyo vitakaa huko, hata siku ile nitakapovijilia, asema Bwana; hapo ndipo nitakapovileta tena, na kuvirudisha mahali hapa.

Yeremia 28

1 Ikawa, katika mwaka ule ule, mwanzo wa kutawala kwake Sedekia, mfalme wa Yuda, mwaka wa nne, mwezi wa tano, Hanania, mwana wa Azuri, nabii, wa Gibeoni, akasema nami ndani ya nyumba ya Bwana, mbele ya makuhani na watu wote, akisema, 2 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimeivunja nira ya mfalme wa Babeli. 3 Kabla haujatimia muda wa miaka miwili mizima, nitavirudisha mahali hapa vyombo vyote vya nyumba ya Bwana, ambavyo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, aliviondoa katika mahali hapa, akavichukua mpaka Babeli. 4 Nami nitamrudisha hapa Yekonia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, pamoja na mateka wote wa Yuda, waliokwenda Babeli, asema Bwana; maana nitaivunja nira ya mfalme wa Babeli. 5 Ndipo nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, mbele ya makuhani, na mbele ya watu wote waliosimama ndani ya nyumba ya Bwana, 6 naam, nabii Yeremia akasema, Amina, Bwana na atende hivi; Bwana ayatimize maneno yako uliyotabiri, kuvirudisha hapa vyombo vya nyumba ya Bwana na watu wote waliofungwa, toka Babeli, hata mahali hapa. 7 Lakini lisikilize sasa neno hili nilisemalo, masikioni mwako, na masikioni mwa watu wote, 8 Manabii waliokuwako kabla ya zamani zangu, na zamani zako, walitabiri juu ya nchi nyingi, na juu ya falme kubwa, habari ya vita, na ya mabaya, na ya tauni. 9 Nabii atabiriye habari za amani, neno la nabii yule litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kuwa Bwana amemtuma kweli kweli. 10 Ndipo nabii Hanania akaitwaa hiyo nira iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, akaivunja. 11 Naye Hanania akanena mbele ya watu wote, akisema, Bwana asema hivi, Hivyo ndivyo nitakavyoivunja nira ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, kabla haujatimia muda wa miaka miwili mizima, na kuiondoa shingoni mwa mataifa yote. Basi nabii Yeremia akaenda zake. 12 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, baada ya Hanania, nabii, kuivunja ile nira iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, kusema, 13 Enenda ukamwambie Hanania, ukisema, Bwana asema hivi, Umezivunja nira za mti; lakini badala yake utafanya nira za chuma. 14 Maana Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimetia nira ya chuma juu ya shingo ya mataifa haya yote, ili wamtumikie Nebukadreza, mfalme wa Babeli nao watamtumikia; nami nimempa wanyama wa nchi pia. 15 Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, Sikia sasa, Ee Hanania; Bwana hakukutuma; lakini unawatumainisha watu hawa maneno ya uongo. 16 Basi Bwana asema hivi, Tazama, nakutuma uende zako toka juu ya uso wa nchi; mwaka huu utakufa, kwa sababu umenena maneno ya uasi juu ya Bwana. 17 Basi nabii Hanania akafa, mwaka uo huo, mwezi wa saba.

Yeremia 29

1 Maneno haya ndiyo maneno ya waraka, ambao nabii Yeremia aliupeleka toka Yerusalemu, kwa hao waliobaki wa wakuu waliochukuliwa mateka, na kwa makuhani, na kwa manabii, na kwa watu wote, ambao Nebukadreza aliwachukua mateka toka Yerusalemu hata Babeli; 2 (hapo walipokwisha kutoka Yerusalemu Yekonia mfalme, na mama yake mfalme, na matowashi, na wakuu wa Yuda na Yerusalemu, na mafundi, na wahunzi;) 3 kwa mkono wa Elasa, mwana wa Shafani, na Gemaria, mwana wa Hilkia, (ambao Sedekia, mfalme wa Yuda, aliwatuma hata Babeli, kwa Nebukadreza, mfalme wa Babeli), kusema, 4 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, awaambia hivi watu wote waliochukuliwa mateka, niliowafanya wachukuliwe toka Yerusalemu mpaka Babeli; 5 Jengeni nyumba, mkakae ndani yake, kapandeni bustani, mkale matunda yake; 6 oeni wake, mkazae wana na binti; kawaozeni wake wana wenu, mkawaoze waume binti zenu, wazae wana na binti; mkaongezeke huko wala msipungue. 7 Kautakieni amani mji ule, ambao nimewafanya mchukuliwe mateka, mkauombee kwa Bwana; kwa maana katika amani yake mji huo ninyi mtapata amani. 8 Maana Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Manabii walio kati yenu, na wabashiri wenu, wasiwadanganye ninyi, wala msisikilize ndoto zenu, mnazootesha. 9 Kwa maana kwa jina langu hutabiri maneno ya uongo kwenu; mimi sikuwatuma, asema Bwana. 10 Maana Bwana asema hivi, Babeli utakapotimiziwa miaka sabini, nitawajilia ninyi, na kulitimiza neno langu jema kwenu, kwa kuwarudisha mahali hapa. 11 Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho. 12 Nanyi mtaniita, mtakwenda na kuniomba, nami nitawasikiliza. 13 Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote. 14 Nami nitaonekana kwenu, asema Bwana, nami nitawarudisha watu wenu waliofungwa, nami nitawakusanya ninyi, nikiwatoa katika mataifa yote, na katika mahali pote, nilikowafukuza, asema Bwana; nami nitawaleta tena, hata mahali ambapo kutoka hapo naliwafanya mchukuliwe mateka. 15 Maana mmesema, Bwana ametuinulia manabii huko Babeli. 16 Maana Bwana asema hivi, katika habari za mfalme aketiye katika kiti cha enzi cha Daudi, na katika habari za watu wote wakaao ndani ya mji huu, ndugu zenu wasiokwenda pamoja nanyi kufungwa; 17 Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama, nitaleta juu yao upanga, na njaa, na tauni, nami nitawafanya kuwa kama tini mbovu, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu sana. 18 Nami nitawafuatia kwa upanga, na njaa, na tauni, nami nitawatoa watupwe huko na huko katika falme zote za dunia, wawe kitu cha kulaaniwa, na cha kushangaza, na cha kuzomewa, na cha kulaumiwa, katika mataifa yote nilikowafukuza. 19 Kwa sababu hawakusikiliza maneno yangu, asema Bwana, ambayo naliwatuma watumishi wangu, hao manabii, nikiamka mapema, na kuwatuma; lakini hamkutaka kusikiliza, asema Bwana. 20 Basi, lisikieni neno la Bwana, ninyi nyote mliochukuliwa mateka, niliowapeleka toka Yerusalemu mpaka Babeli. 21 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, katika habari za Ahabu, mwana wa Kolaya, na katika habari za Sedekia, mwana wa Maaseya, wawatabiriao ninyi maneno ya uongo kwa jina langu; Tazama, nitawatia katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, naye atawaua mbele ya macho yenu. 22 Tena katika habari zao laana itatumiwa na wafungwa wote wa Yuda, walioko Babeli, kusema, Bwana akufanye uwe kama Sedekia, na kama Ahabu, ambao mfalme wa Babeli aliwaoka motoni; 23 kwa sababu wametenda upumbavu katika Israeli, nao wamezini na wake za jirani zao, nao wamenena maneno ya uongo kwa jina langu, nisiyowaamuru; nami ndimi nijuaye, nami ni shahidi, asema Bwana. 24 Na katika habari za Shemaya, Mnehelami, utanena, ukisema, 25 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, ya kwamba, Kwa kuwa kwa jina lako mwenyewe umewapelekea barua watu wote walioko Yerusalemu, na Sefania, mwana wa Maaseya, kuhani, na makuhani wote, kusema, 26 Bwana amekufanya kuhani badala ya Yehoyada, kuhani, ili mpate kuwa watumishi katika nyumba ya Bwana, kwa kila mtu aliye na wazimu, na kwa kila mtu ajifanyaye kuwa nabii, umtie katika mkatale na pingu. 27 Mbona, basi, hukumkemea Yeremia wa Anathothi, ajifanyaye kuwa nabii kwenu, 28 ambaye ametuma watu kwetu katika Babeli, kusema, Uhamisho huu ni wa siku nyingi; jengeni nyumba, mkakae ndani yake; pandeni bustani, mkale matunda yake. 29 Na Sefania, kuhani, akasoma barua hii masikioni mwa Yeremia nabii. 30 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema, 31 Uwapelekee habari watu wote waliohamishwa, kusema, Bwana asema hivi, katika habari za Shemaya, Mnehelami; Kwa sababu Shemaya amewatabiria ninyi, lakini sikumtuma mimi, naye amewatumainisha neno la uongo; 32 basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitamwadhibu Shemaya, Mnehelami, na wazao wake; hatakuwa na mtu atakayekaa katika watu hawa, wala hatayaona mema nitakayowatendea watu wangu, asema Bwana; kwa sababu amenena maneno ya uasi juu ya Bwana.

Yeremia 30

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 2 Bwana Mungu wa Israeli, asema hivi, ya kwamba, Uyaandike kitabuni maneno hayo yote niliyokuambia. 3 Kwa maana, tazama, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapowarejeza watu wangu wa Israeli na Yuda waliofungwa, asema Bwana; nami nitawarudisha hata nchi niliyowapa baba zao, nao wataimiliki. 4 Na haya ndiyo maneno aliyosema Bwana, katika habari za Israeli, na katika habari za Yuda. 5 Maana Bwana asema hivi, Tumesikia sauti ya tetemeko, na ya hofu, wala si ya amani. 6 Ulizeni sasa, mkaone kwamba mwanamume aona utungu wa uzazi; mbona, basi, ninaona kila mtu anaweka mikono yake viunoni, kama mwanamke aliye na utungu, na nyuso zote zimegeuka rangi. 7 Ole! Maana siku ile ni kuu, hata hapana inayofanana nayo, maana ni wakati wa taabu yake Yakobo; lakini ataokolewa nayo. 8 Na itakuwa katika siku ile, asema Bwana wa majeshi, nitaivunja nira yake itoke shingoni mwako, nami nitavipasua vifungo vyako; wala wageni hawatamtumikisha tena; 9 bali watamtumikia Bwana, Mungu wao, na Daudi, mfalme wao, nitakayemwinua kwa ajili yao. 10 Kwa sababu hiyo usiogope, Ee Yakobo, mtumishi wangu, asema Bwana; wala usifadhaike, Ee Israeli; kwa maana, tazama, nitakuokoa toka mbali, na wazao wako toka nchi ya uhamisho wao; na Yakobo atarudi, naye atatulia na kustarehe, wala hapana mtu atakayemtia hofu. 11 Maana mimi ni pamoja nawe, asema Bwana, nikuokoe; maana nitawakomesha kabisa mataifa yote huko nilikokutawanya, bali sitakukomesha wewe kabisa; lakini nitakurudi kwa hukumu, wala sitakuacha bila adhabu. 12 Maana Bwana asema hivi, Maumivu yako hayaponyekani, na jeraha yako ni kubwa. 13 Hapana mtu wa kukutetea; kwa jeraha yako huna dawa ziponyazo. 14 Wote wakupendao wamekusahau; hawakutafuti; maana nimekujeruhi kwa jeraha ya adui, kwa adhabu ya mtu mkatili; kwa sababu ya ukubwa wa uovu wako, kwa sababu dhambi zako zilikuwa zimeongezeka. 15 Mbona unalilia maumivu yako? Hayaponyeki maumivu yako; kwa sababu ya ukubwa wa uovu wako, kwa sababu dhambi zako zimeongezeka, nimekutenda haya. 16 Basi, watu wote wakulao wataliwa; na adui zako wote watakwenda kufungwa; kila mmoja wao; na hao waliokuteka nyara watatekwa; na wote waliokuwinda nitawafanya kuwa mawindo. 17 Maana nitakurudishia afya, nami nitakuponya jeraha zako, asema Bwana, kwa sababu wamekuita, mwenye kutupwa, wakisema, Ni Sayuni, ambao hapana mtu autakaye. 18 Bwana asema hivi, Tazama, nitarudisha tena hema za Yakobo zilizohamishwa, na kuyahurumia makao yake; nao mji huo utajengwa juu ya magofu yake wenyewe, nalo jumba litakaliwa, kama ilivyokuwa desturi yake. 19 Tena kwao itasikiwa shukrani, na sauti yao wachangamkao; nami nitawazidisha, wala hawatakuwa wachache; tena nitawatukuza, wala hawatakuwa wanyonge. 20 Watoto wao nao watakuwa kama zamani, na kusanyiko lao litathibitika mbele zangu, nami nitawaadhibu wote wawaoneao. 21 Na mkuu wao atakuwa mtu wa kwao wenyewe, naye mwenye kuwatawala atakuwa mtu wa jamaa yao; nami nitamkaribisha, naye atanikaribia; maana ni nani aliye na moyo wa kuthubutu kunikaribia? Asema Bwana. 22 Nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. 23 Tazama, tufani ya Bwana, yaani, ghadhabu yake, imetokea tufani ya kudumu; itawaangukia waovu vichwani. 24 Hasira kali ya Bwana haitarudi, hata atakapokwisha kutenda, hata atakapokwisha kuyatimiza makusudi ya moyo wake; katika siku za mwisho mtayafahamu haya.

Yeremia 31

1 Wakati huo, asema Bwana, nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Israeli, nao watakuwa watu wangu. 2 Bwana asema hivi, Watu wale walioachwa na upanga walipata neema jangwani; yaani, Israeli, hapo nilipokwenda kumstarehesha. 3 Bwana alinitokea zamani, akisema, Naam nimekupenda kwa upendo wa milele, ndiyo maana nimekuvuta kwa fadhili zangu. 4 Mara ya pili nitakujenga, nawe utajengwa, Ee bikira wa Israeli mara ya pili utapambwa kwa matari yako, nawe utatokea katika michezo yao wanaofurahi. 5 Mara ya pili utapanda mizabibu juu ya milima ya Samaria; wapanzi watapanda, nao watayafurahia matunda yake. 6 Maana kutakuwa siku moja, ambayo walinzi watalia juu ya vilima vya Efraimu, Inukeni, tukaende Sayuni, kwa Bwana, Mungu wetu. 7 Maana Bwana asema hivi, Mwimbieni Yakobo kwa furaha, mkampigie kelele mkuu wa mataifa, tangazeni, sifuni, mkaseme, Ee Bwana, uwaokoe watu wako, mabaki ya Israeli. 8 Tazama, nitawaleta toka nchi ya kaskazini, na kuwakusanya katika miisho ya dunia, na pamoja nao watakuja walio vipofu, na hao wachechemeao, mwanamke mwenye mimba, na yeye pia aliye na utungu wa kuzaa; watarudi huko, jeshi kubwa. 9 Watakuja kwa kulia, na kwa maombi nitawaongoza; nitawaendesha penye mito ya maji, katika njia iliyonyoka; katika njia hiyo hawatajikwaa; maana mimi ni baba wa Israeli, na Efraimu ni mzaliwa wa kwanza wangu. 10 Lisikieni neno la Bwana, enyi mataifa, litangazeni visiwani mbali; mkaseme, Aliyemtawanya Israeli atamkusanya, na kumlinda, kama mchungaji alindavyo kundi lake. 11 Kwa maana Bwana amemweka huru Yakobo, amemkomboa mkononi mwake aliyekuwa hodari kuliko yeye. 12 Nao watakuja, na kuimba katika mlima Sayuni, wataukimbilia wema wa Bwana, nafaka, na divai, na mafuta, na wachanga wa kondoo na wa ng'ombe; na roho zao zitakuwa kama bustani iliyotiwa maji; wala hawatahuzunika tena kabisa. 13 Ndipo bikira atafurahi katika kucheza, na vijana na wazee pamoja; maana nitageuza masikitiko yao kuwa furaha, nami nitawafariji, na kuwafurahisha waache huzuni zao. 14 Nami nitaishibisha roho ya makuhani kwa unono, na watu wangu watashiba kwa wema wangu, asema Bwana 15 Bwana asema hivi, Sauti imesikiwa Rama, kilio, na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake; asikubali kufarijiwa kwa watoto wake, kwa kuwa hawako, 16 Bwana asema hivi, Zuia sauti yako, usilie, na macho yako yasitoke machozi; Maana kazi yako itapata thawabu, nao watakuja tena toka nchi ya adui; Ndivyo asemavyo Bwana. 17 Tena liko tumaini kwa siku zako za mwisho, asema Bwana; na watoto wako watarejea hata mpaka wao wenyewe. 18 Hakika nimemsikia Efraimu, akijililia hivi, Umeniadhibu, nami nikaadhibika, kama ndama asiyeizoelea nira; unigeuze, nami nitageuzwa; kwa maana wewe u Bwana, Mungu wangu. 19 Hakika baada ya kugeuzwa kwangu, nalitubu; na baada ya kufundishwa kwangu, nalijipiga pajani; nalitahayarika, naam, nalifadhaika, kwa sababu naliichukua aibu ya ujana wangu. 20 Je! Efraimu siye mwanangu mpendwa? Je! Siye mtoto apendezaye? Maana kila nisemapo neno juu yake, ningali nikimkumbuka sana; kwa sababu hiyo moyo wangu unataabika kwa ajili yake; bila shaka nitamrehemu, asema Bwana. 21 Jiwekee alama za njia; jifanyie miti ya kukuongoza; uuelekeze moyo wako kwenye njia kuu, njia ile ile uliyoiendea; rudi tena, Ee bikira wa Israeli, irudie hii miji yako. 22 Hata lini utatanga-tanga, Ee binti mwenye kuasi? Kwa maana Bwana ameumba jambo jipya duniani; mwanamke atamlinda mwanamume. 23 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Watatumia tena neno hili katika nchi ya Yuda, na katika miji yake, nitakapowarudisha mateka yao; Bwana na akubariki, Ee kao la haki, Ee mlima wa utakatifu. 24 Na Yuda, na miji yake yote, watakaa humo pamoja; wakulima, nao waendao huko na huko pamoja na makundi yao. 25 Kwa maana nimeishibisha roho yenye uchovu, nami nimeiridhisha kila roho yenye huzuni. 26 Basi, nikaamka, nikaangalia; na usingizi wangu ulikuwa mtamu kwangu. 27 Tazama, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapoipanda nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda, mbegu ya mwanadamu na mbegu ya mnyama. 28 Tena itakuwa, kwa kadiri nilivyowaangalia, ili kung'oa, na kubomoa, na kuangusha, na kuangamiza, na kutesa; kwa kadiri iyo hiyo nitawaangalia, ili kujenga, na kupanda, asema Bwana. 29 Siku zile, hawatasema tena, Baba za watu wamekula zabibu kali, na meno ya watoto wao yametiwa ganzi. 30 Bali kila mtu atakufa kwa sababu ya uovu wake mwenyewe; kila mtu alaye zabibu kali, meno yake yatatiwa ganzi. 31 Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. 32 Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono, ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa nalikuwa mume kwao, asema Bwana. 33 Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema Bwana; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. 34 Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue Bwana; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema Bwana; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena. 35 Bwana asema hivi, awapaye watu jua, ili kuwa nuru wakati wa mchana, na amri za mwezi na nyota, ili kuwa nuru wakati wa usiku, aichafuaye bahari, hata mawimbi yake yakavuma; Bwana wa majeshi, ndilo jina lake; 36 Amri hizi zikiondoka, zisiwe mbele zangu, asema Bwana, ndipo wazao wa Israeli nao wataacha kuwa taifa mbele zangu milele. 37 Bwana asema hivi, Kama mbingu zikiweza kupimwa, na misingi ya dunia ikiweza kugunduliwa huko chini, ndipo wazao wa Israeli pia nitawatupilia mbali, kwa ajili ya hayo yote waliyoyatenda, asema Bwana. 38 Tazama, siku zinakuja, asema Bwana, mji huu utakapojengwa kwa ajili ya Bwana, toka buruji ya Hananeli hata lango la pembeni. 39 Na kamba ya kupimia itaendelea moja kwa moja hata mlima Garebu, tena itazunguka na kufika Goa. 40 Na bonde lote la mizoga, na majivu, na mashamba yote mpaka kijito Kidroni, mpaka pembe ya lango la farasi, upande wa mashariki, patakuwa patakatifu kwa Bwana; hapatang'olewa, wala hapatabomolewa, hata milele.

Yeremia 32

2 Basi, wakati huo jeshi la mfalme wa Babeli liliuzunguka Yerusalemu; na Yeremia, nabii, alikuwa amefungwa ndani ya uwanda wa walinzi, uliokuwa katika nyumba ya mfalme wa Yuda. 3 Kwa maana Sedekia, mfalme wa Yuda, alikuwa amemfunga, akisema, Kwa nini unatabiri, na kusema, Bwana asema hivi, Angalia, nitatia mji huu katika mikono ya mfalme wa Babeli, naye atautwaa; 4 tena, Sedekia, mfalme wa Yuda, hatapona kutoka katika mikono ya Wakaldayo, lakini hakika yake atatiwa katika mikono ya mfalme wa Babeli, atanena naye mdomo kwa mdomo, na macho yake yatatazama macho yake; 5 naye atamchukua Sedekia mpaka Babeli, naye atakuwako huko hata nitakapomjilia, asema Bwana; mjapopigana na Wakaldayo hamtafanikiwa. 6 Yeremia akasema, Neno la Bwana limenijia, kusema, 7 Tazama, Hanameli, mwana wa Shalumu, mjomba wako, atakujia, akisema, Jinunulie shamba langu lililoko Anathothi; maana haki ya ukombozi ni yako, ulinunue. 8 Basi Hanameli, mwana wa mjomba wangu, akanijia ndani ya uwanda wa walinzi, sawasawa na lile neno la Bwana, akaniambia, Tafadhali, ulinunue shamba langu lililoko Anathothi, katika nchi ya Benyamini; maana haki ya urithi ni yako, na haki ya ukombozi ni yako; ujinunulie. Ndipo nikajua kama neno hili ni neno la Bwana. 9 Basi nikalinunua shamba lile lililoko Anathothi kwa Hanameli, mwana wa mjomba wangu, nikampimia fedha yake, shekeli kumi na saba za fedha. 10 Nami nikaitia sahihi ile hati, na kuipiga muhuri, nikawaita mashahidi, nikampimia ile fedha katika mizani. 11 Nikaitwaa ile hati ya kununua, ile iliyopigwa muhuri kama ilivyo sheria na ada, na ile nayo iliyokuwa wazi; 12 na ile hati ya kununua nikampa Baruku, mwana wa Neria, mwana wa Maaseya, mbele ya uso wa Hanameli, mwana wa mjomba wangu, na mbele ya mashahidi wale walioitia sahihi hati ya kununua, mbele ya Wayahudi wote walioketi katika uwanda wa walinzi. 13 Nami nikamwagiza Baruku mbele yao, nikisema, 14 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Twaa hati hizi, hati hii ya kununua, hati hii iliyopigwa muhuri, na hii iliyo wazi pia, ukazitie katika chombo cha udongo, zipate kukaa siku nyingi. 15 Maana Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nyumba na mashamba na mashamba ya mizabibu yatanunuliwa tena katika nchi hii. 16 Hata nikiisha kumpa Baruku, mwana wa Neria, hati ile ya kununua, nalimwomba Bwana, nikisema, 17 Aa! Bwana MUNGU, tazama, wewe umeziumba mbingu na nchi, kwa uweza wako mkuu na kwa mkono wako ulionyoshwa; hapana neno lililo gumu usiloliweza; 18 wewe uwarehemuye watu elfu nyingi, uwalipaye baba za watu uovu wao vifuani mwa watoto wao baada yao; Mungu aliye mkuu, aliye hodari, Bwana wa majeshi ndilo jina lake; 19 mkuu wa mashauri, mweza katika kutenda; ambaye macho yake yamefumbuka juu ya njia zote za wanadamu, kumpa kila mtu kwa kadiri ya njia zake, na kwa kadiri ya matunda ya matendo yake, 20 wewe uliyeweka ishara na ajabu katika nchi ya Misri hata siku hii ya leo, katika Israeli na kati ya watu wengine; na kujifanyia jina kama ilivyo leo; 21 ukawatoa watu wako, Israeli, katika nchi ya Misri, kwa ishara, na kwa ajabu, na kwa mkono hodari, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mkuu; 22 ukawapa nchi hii, uliyowaapia baba zao kwamba utawapa, nchi iliyojaa maziwa na asali; 23 nao wakaingia, wakaimiliki; lakini hawakuitii sauti yako, wala hawakuenda katika sheria yako; hawakutenda neno lo lote katika haya uliyowaagiza wayatende; basi, kwa sababu hii umeleta juu yao mabaya haya yote; 24 angalia maboma haya; wameujia mji huu ili kuutwaa; na mji huu umetiwa katika mikono ya Wakaldayo wanaopigana nao, kwa sababu ya upanga, na njaa, na tauni; na hayo uliyosema yamekuwa; na, tazama, wewe unayaona. 25 Nawe, Ee Bwana MUNGU, umeniambia, Jinunulie shamba lile kwa fedha, ukawaite mashahidi; iwapo mji huu umetiwa katika mikono ya Wakaldayo; je! Itakuwaje? 26 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema, 27 Tazama, mimi ni Bwana, Mungu wa wote wenye mwili; je! Kuna neno gumu lo lote nisiloliweza? 28 Basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitautia mji huu katika mikono ya Wakaldayo, na katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, naye atautwaa; 29 na Wakaldayo, wanaopigana na mji huu, watakuja, na kuutia moto mji huu, na kuuteketeza, pamoja na nyumba zake, ambazo juu ya dari zake wamemfukizia Baali uvumba, na kuwamiminia miungu mingine vinywaji, ili kunikasirisha. 30 Maana wana wa Israeli, na wana wa Yuda, wametenda yaliyo mabaya tu mbele za uso wangu, tangu ujana wao; maana wana wa Israeli wamenichokoza tu kwa matendo ya mikono yao, asema Bwana. 31 Kwa kuwa mji huu umekuwa sababu ya kunitia hasira, na sababu ya ghadhabu yangu, tangu siku ile walipoujenga hata siku hii ya leo; ili niuondoe usiwe mbele za uso wangu; 32 kwa sababu ya mabaya yote ya wana wa Israeli, na ya wana wa Yuda, waliyoyatenda ili kunitia hasira, wao, na wafalme wao, na wakuu wao, na makuhani wao, na manabii wao, na watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu. 33 Tena wamenigeuzia visogo vyao, wala si nyuso zao; ingawa naliwafundisha, niliondoka mapema na kuwafundisha, lakini hawakusikiliza ili wapate mafundisho. 34 Bali waliweka machukizo yao ndani ya nyumba iliyoitwa kwa jina langu, ili kuinajisi. 35 Tena walijenga mahali palipoinuka kwa Baali, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwapitisha wana wao na binti zao katika moto kwa ajili ya Moleki, jambo nisilowaagiza; wala halikuingia moyoni mwangu kwamba walitende chukizo hilo; wapate kumkosesha Yuda. 36 Basi sasa, Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, katika habari za mji huu, ambao ninyi mnasema juu yake maneno haya, Umetiwa katika mikono ya mfalme wa Babeli, kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; 37 Tazama, nitawakusanya, na kuwatoa katika nchi zote nilikowafukuza, katika hasira yangu, na uchungu wangu, na ghadhabu yangu nyingi; nami nitawaleta tena hata mahali hapa, nami nitawakalisha salama salimini; 38 nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; 39 nami nitawapa moyo mmoja na njia moja, wapate kunicha sikuzote; kwa mema yao, na ya watoto wao baada yao; 40 nami nitafanya agano la milele pamoja nao, kwamba sitageuka wala kuwaacha, ili niwatendee mema; nami nitatia kicho changu mioyoni mwao, ili wasiniache. 41 Naam, nitafurahi juu yao niwatendee mema, nami nitawapanda katika nchi hii kweli kweli, kwa moyo wangu wote, na kwa roho yangu yote. 42 Maana Bwana asema hivi, Kama nilivyoleta mabaya makuu haya yote juu ya watu hawa, vivyo hivyo nitaleta juu yao mema hayo yote niliyowaahidia. 43 Na mashamba yatanunuliwa katika nchi hii, mnayoitaja, mkisema, Ni ukiwa, haina mwanadamu wala mnyama; imetiwa katika mikono ya Wakaldayo. 44 Watu watanunua mashamba kwa fedha, watazitia sahihi hati zake, na kuzipiga muhuri, na kuwaita mashahidi, katika nchi ya Benyamini, na katika mahali palipo pande zote za Yerusalemu, na katika miji ya Yuda, na katika miji ya nchi yenye vilima, na katika miji ya nchi tambarare, na katika miji ya Negebu; kwa maana nitawarudisha wafungwa wao, asema Bwana.

Yeremia 33

2 Bwana alitendaye jambo hili, Bwana aliumbaye ili alithibitishe; Bwana ndilo jina lake; asema hivi, 3 Niite, nami nitakuitikia, nami nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua. 4 Maana Bwana, Mungu wa Israeli asema hivi, katika habari za nyumba za mji huu, na katika habari za nyumba za wafalme wa Yuda, zilizobomolewa ili kuyapinga maboma na upanga; 5 Wanakuja kupigana na Wakaldayo, lakini ni kuzijaza kwa mizoga ya watu, niliowaua katika hasira yangu na ghadhabu yangu, ambao kwa ajili ya uovu wao wote nimeuficha mji huu uso wangu. 6 Tazama, nitauletea afya na kupona, nami nitawaponya; nami nitawafunulia wingi wa amani na kweli. 7 Nami nitawarudisha wafungwa wa Yuda, na wafungwa wa Israeli, na kuwajenga kama kwanza. 8 Nami nitawasafisha na uovu wao wote, ambao kwa huo wamenitenda dhambi; nami nitawasamehe maovu yao yote, ambayo kwayo wamenitenda dhambi, na kukosa juu yangu. 9 Na mji huu utakuwa kwangu jina la furaha, na sifa na utukufu, mbele ya mataifa yote ya dunia, watakaosikia habari ya mema yote niwatendeayo, nao wataogopa na kutetemeka, kwa sababu ya mema yote na amani nitakaoupatia mji huo. 10 Bwana asema hivi, katika mahali hapo ambapo mnasema kwamba ni ukiwa, hapana mwanadamu wala mnyama, naam, katika miji ya Yuda na katika njia za Yerusalemu, zilizo ukiwa, hazina mwanadamu wala mwenyeji wala mnyama, 11 itasikilikana tena sauti ya furaha na sauti ya shangwe, sauti ya bwana arusi na sauti ya bibi arusi, sauti yao wasemao Mshukuruni Bwana wa majeshi, maana Bwana ni mwema, rehema zake ni za milele; na sauti zao waletao sadaka za shukrani nyumbani kwa Bwana. Kwa kuwa nitawarudisha wafungwa wa nchi hii kama kwanza, asema Bwana. 12 Bwana wa majeshi asema hivi, Katika mahali hapa, palipo ukiwa, hapana mwanadamu wala mnyama, na katika miji yake yote, yatakuwapo makao ya wachungaji wakizilaza kondoo zao. 13 Katika miji ya nchi ya vilima, katika miji ya nchi tambarare, katika miji ya Negebu, na katika nchi ya Benyamini, na katika mahali palipo karibu na Yerusalemu, na katika miji ya Yuda, makundi ya kondoo yatapita tena chini ya mikono yake awahesabuye, asema Bwana. 14 Tazama, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapolitimiza neno lile jema nililolinena, katika habari za nyumba ya Israeli, na katika habari za nyumba ya Yuda. 15 Katika siku zile, na wakati ule, nitamchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atafanya hukumu na haki katika nchi hii. 16 Katika siku zile Yuda ataokolewa, na Yerusalemu utakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu. 17 Maana Bwana asema hivi, Daudi hatakosa kuwa na mtu wa kuketi katika kiti cha enzi cha nyumba ya Israeli; 18 wala makuhani Walawi hawatakosa kuwa na mtu wa kusimama mbele zangu, na kutoa sadaka za kuteketezwa, na kufukiza matoleo, na kufanya dhabihu daima. 19 Neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema, 20 Bwana asema hivi, Kama mkiweza kulivunja agano langu la mchana, na agano langu la usiku, hata usiwepo tena mchana na usiku kwa wakati wake, 21 ndipo agano langu nililolifanya na Daudi, mtumishi wangu, laweza kuvunjika, hata asiwe na mwana wa kumiliki katika kiti chake cha enzi; tena agano langu nililofanya na Walawi makuhani, wahudumu wangu, laweza kuvunjika. 22 Kama vile jeshi la mbinguni haliwezi kuhesabiwa, wala mchanga wa bahari kupimwa; ndivyo nitakavyoongeza wazao wa Daudi, mtumishi wangu, na Walawi wanaonihudumia. 23 Kisha neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema, 24 Je! Hufikiri neno hili walilolisema watu hawa, wakinena, Jamaa zile mbili alizozichagua Bwana amezitupilia mbali? Hivyo ndivyo wanavyowadharau watu wangu, ili wasiwe taifa tena mbele yao. 25 Bwana asema hivi, Ikiwa agano langu la mchana na usiku halikai imara, ikiwa mimi sikuziamuru kawaida za mbingu na dunia; 26 ndipo nitawatupilia mbali wazao wa Yakobo, na Daudi, mtumishi wangu, hata nisitwae wazao wake watawale juu ya wazao wa Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo; kwa maana nitawarudisha wafungwa wao, nami nitawarehemu.

Yeremia 34

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, hapo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na jeshi lake lote, na falme zote za dunia zilizokuwa chini ya mamlaka yake, na kabila zote za watu, walipopigana na Yerusalemu, na miji yake yote, kusema, 2 Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Enenda ukaseme na Sedekia, mfalme wa Yuda, ukamwambie, Bwana asema hivi, Tazama, nitatia mji huu katika mikono ya mfalme wa Babeli, naye atauteketeza kwa moto; 3 tena wewe hutaokoka mkononi mwake, lakini utakamatwa kweli kweli, na kutiwa katika mikono yake; na macho yako yatayatazama macho ya mfalme wa Babeli, naye atasema nawe mdomo kwa mdomo, nawe utakwenda Babeli. 4 Hata hivyo lisikie neno la Bwana, Ee Sedekia, mfalme wa Yuda; Bwana asema hivi katika habari zako; hutakufa kwa upanga; 5 utakufa katika amani; na kwa mafukizo ya baba zako, wafalme wa zamani waliokutangulia, ndivyo watakavyokufukizia; nao watakulilia, Aa, Bwana! Kwa maana mimi nimelinena neno hili, asema Bwana. 6 Basi Yeremia, nabii, akamwambia Sedekia, mfalme wa Yuda, maneno hayo yote katika Yerusalemu, 7 wakati ule jeshi la Babeli walipopigana na Yerusalemu na miji yote ya Yuda iliyosalia, na Lakishi, na Azeka; kwa maana miji hiyo tu ndiyo iliyosalia katika miji ya Yuda yenye maboma. 8 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, baada ya wakati ule mfalme Sedekia alipofanya agano na watu wote waliokuwa katika Yerusalemu, kuwatangazia habari ya uhuru; 9 ya kwamba kila mtu amweke huru mtumwa wake, na kila mtu amweke huru mjakazi wake, ikiwa yule mwanamume au yule mwanamke ni Mwebrania; mtu ye yote asiwatumikishe, yaani, asimtumikishe Myahudi, nduguye; 10 na wakuu wote, na watu wote, wakati, waliofanya agano hilo, ya kwamba kila mtu amweke huru mtumwa wake na mjakazi wake, mtu ye yote asiwatumikishe tena; wakatii, wakawaacha. 11 Lakini baadaye wakaghairi, wakawarudisha watumwa wale, na wajakazi wale, ambao wamewaacha huru, nao wakawatia utumwani wawe watumwa na wajakazi wao. 12 Basi, neno la Bwana likamjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 13 Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nalifanya agano na baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa, nikisema, 14 Mwisho wa kila mwaka wa saba kila mtu na amweke huru ndugu yake aliye Mwebrania, aliyeuzwa kwako na kukutumikia miaka sita utamwacha atoke kwako huru, lakini baba zenu hawakunisikiliza, wala hawakutega masikio yao. 15 Na ninyi mlikuwa mmegeuka, mkafanya yaliyo haki machoni pangu, kwa kumtangazia uhuru kila mtu ndugu yake; nanyi mlikuwa mmefanya agano mbele zangu, katika nyumba ile iitwayo kwa jina langu; 16 lakini mlighairi, na kulitukana jina langu; kila mtu akamrudisha mtumwa wake na mjakazi wake, ambao mmewaweka huru kama walivyopenda wenyewe, mkawatia utumwani tena, wawe watumwa wenu na wajakazi wenu. 17 Basi Bwana asema hivi, Hamkunisikiliza kumtangazia uhuru kila mtu ndugu yake, na kila mtu jirani yake; tazama, mimi nawatangazieni uhuru, asema Bwana, yaani, wa upanga, na njaa, na tauni; nami nitawatoa ninyi mtupwe huko na huko katika falme zote za dunia. 18 Na watu hao waliolivunja agano langu, wasioyatimiza maneno ya agano lile, walilolifanya mbele zangu, wakati ule walipomkata ndama vipande viwili, wakapita katikati ya vipande vile; 19 wakuu wa Yuda, na wakuu wa Yerusalemu, matowashi, na makuhani, na watu wote wa nchi, waliopita katikati ya vipande vile vya huyo ndama; 20 mimi nitawatia katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao, na mizoga yao itakuwa ni chakula cha ndege za mbinguni, na cha wanyama wakali wa nchi. 21 Na Sedekia, mfalme wa Yuda, na wakuu wake nitawatia katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao, na katika mikono ya jeshi la mfalme wa Babeli, waliokwenda zao na kuwaacheni. 22 Tazama, nitawapa amri yangu, asema Bwana, na kuwarejeza kwenye mji huu; nao watapigana nao, na kuutwaa, na kuuteketeza kwa moto; nami nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa, isikaliwe na mtu.

Yeremia 35

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, katika siku za Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, kusema, 2 Enenda nyumbani kwa Warekabi, ukanene nao, ukawalete nyumbani kwa Bwana, katika chumba kimoja, ukawape divai wanywe. 3 Basi nikamtwaa Yaazania, mwana wa Yeremia, mwana wa Habasinia, na ndugu zake, na wanawe wote, na nyumba yote ya Warekabi; 4 nikawaleta ndani ya nyumba ya Bwana, ndani ya chumba cha wana wa Hanani, mwana wa Igdalia, mtu wa Mungu, kilichokuwa karibu na chumba cha wakuu, nacho kilikuwa juu ya chumba cha Maaseya, mwana wa Shalumu, bawabu; 5 nikaweka mabakuli yaliyojaa divai, na vikombe, mbele ya wana wa nyumba ya Warekabi, nikawaambia, Nyweni divai. 6 Lakini wakasema, Hatutakunywa divai; kwa maana Yonadabu, mwana wa Rekabu, baba yetu, alituamuru, akisema, Msinywe divai, ninyi wala wana wenu, hata milele; 7 wala msijenge nyumba, wala msipande mbegu, wala msipande mizabibu, wala msiwe nayo; bali siku zenu zote mtakaa katika hema; mpate kuishi siku nyingi katika nchi ambayo mtakaa ndani yake hali ya wageni. 8 Nasi tumeitii sauti ya Yonadabu, mwana wa Rekabu, baba yetu, katika yote aliyotuamuru, kwamba tusinywe divai siku zetu zote, sisi, na wake zetu, na wana wetu, na binti zetu; 9 wala tusijijengee nyumba za kukaa; wala hatuna shamba la mizabibu, wala konde, wala mbegu; 10 bali tumekaa katika hema, nasi tumetii; tukafanya sawasawa na yote aliyotuamuru Yonadabu, baba yetu. 11 Lakini ikawa, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alipopanda akaingia nchi hii, ndipo tukasema, Haya! Twende Yerusalemu, tukiliogopa jeshi la Wakaldayo, na tukiliogopa jeshi la Washami; basi hivyo tunakaa Yerusalemu. 12 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema, 13 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Enenda ukawaambie wana wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, Je! Hamtaki kupokea mafundisho, myasikilize maneno yangu? Asema Bwana. 14 Maneno ya Yonadabu, mwana wa Rekabu, aliyowaamuru wanawe, kwamba wasinywe divai, yametimizwa, na hata leo hawanywi; maana waitii hiyo amri ya baba yao; lakini mimi nimesema nanyi, nikiamka mapema na kunena, bali ninyi hamkunisikiliza mimi. 15 Pia naliwapeleka watumishi wangu wote, manabii, kwenu ninyi, nikiamka mapema na kuwapeleka, nikisema, Rudini sasa, kila mtu na aiache njia yake mbaya, mkatengeneze matendo yenu, wala msiwafuate miungu mingine, ili kuwatumikia, nanyi mtakaa katika nchi hii, niliyowapa ninyi na baba zenu; lakini hamkutega masikio yenu, wala hamkunisikiliza. 16 Basi, kwa kuwa wana wa Yonadabu, mwana wa Rekabu, wameitimiza amri ya baba yao aliyowaamuru, lakini watu hawa hawakunisikiliza mimi; 17 kwa sababu hiyo, asema Bwana, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli; Tazama nitaleta juu ya Yuda, na juu ya wenyeji wote wa Yerusalemu, mabaya yote niliyoyatamka juu yao; kwa sababu nimesema nao, wasinisikilize; nimewaita, wala hawakuniitikia. 18 Naye Yeremia akawaambia watu wa nyumba ya Warekabi, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa sababu mmeitii amri ya Yonadabu, baba yenu, na kuyashika maagizo yake yote, na kutenda sawasawa na yote aliyowaamuru; 19 basi, kwa sababu hiyo, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Yonadabu, mwana wa Rekabu, hatakosa kuwa na mtu wa kusimama mbele zangu hata milele.

Yeremia 36

1 Ikawa katika mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili likamjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, 2 Twaa gombo la chuo, ukaandike ndani yake maneno yote niliyokuambia juu ya Israeli, na juu ya Yuda, na juu ya mataifa yote, tangu siku ile niliponena nawe, tangu siku za Yosia, hata siku hii ya leo. 3 Huenda nyumba ya Yuda watasikia mabaya yote niliyokusudia kuwatenda; wapate kurudi, kila mtu akaiache njia yake mbaya; nami nikawasamehe uovu wao na dhambi yao. 4 Kisha Yeremia akamwita Baruku, mwana wa Neria; naye Baruku akaandika katika gombo la chuo maneno yote ya Bwana, yaliyotoka kinywani mwa Yeremia, ambayo Bwana amemwambia. 5 Yeremia akamwagiza Baruku, ya kwamba, Mimi nimefungwa, siwezi kuingia katika nyumba ya Bwana. 6 Basi, enenda wewe, ukasome katika gombo la chuo, ambacho umeandika ndani yake, maneno ya Bwana yaliyotoka kinywani mwangu, ukiyasoma katika masikio ya watu, ndani ya nyumba ya Bwana, siku ya kufunga; pia utayasoma masikioni mwa watu wote wa Yuda, watokao katika miji yao. 7 Labda wataomba dua zao mbele za Bwana, na kurudi, kila mtu akiiacha njia yake mbaya; kwa maana hasira na ghadhabu ni kuu sana, alizotamka Bwana juu ya watu hawa. 8 Basi, Baruku, mwana wa Neria, akafanya sawasawa na hayo yote, ambayo Yeremia, nabii, amemwagiza, akisoma katika chuo hicho, maneno ya Bwana, ndani ya nyumba ya Bwana. 9 Basi, ikawa katika mwaka wa tano wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, katika mwezi wa kenda, watu wote waliokuwa katika Yerusalemu, na watu wote waliokuja Yerusalemu kutoka miji yote ya Yuda, wakapiga mbiu ya kufunga mbele za Bwana. 10 Basi, wakati huo Baruku akayasoma maneno ya Yeremia katika nyumba ya Bwana, katika chumba cha Gemaria, mwana wa Shafani, mwandishi, katika ua wa juu, mahali pa kuingilia kwa lango jipya la nyumba ya Bwana, akiyasoma katika masikio ya watu wote. 11 Basi, Mikaya, mwana wa Gemaria, mwana wa Shafani, aliposikia maneno yote ya Bwana yaliyokuwa katika chuo hicho, 12 akashuka, akaingia katika nyumba ya mfalme, katika chumba cha mwandishi, na, tazama, wakuu wote wameketi humo, nao ni hawa, Elishama, mwandishi, na Delaya, mwana wa Shemaya, na Elnathani, mwana wa Akbori, na Gemaria, mwana wa Shafani, na Sedekia, mwana wa Hanania, na wakuu wote. 13 Naye Mikaya akawaeleza maneno yote aliyoyasikia, hapo Baruku alipokuwa akikisoma kitabu masikioni mwa watu. 14 Basi, wakuu wote wakamtuma Yehudi, mwana wa Nethania, mwana wa Shelemia, mwana wa Kushi, aende kwa Baruku, kumwambia, Litwae mkononi mwako gombo lile ulilolisoma masikioni mwa watu, uje huku. Basi, Baruku, mwana wa Neria, akalitwaa gombo lile mkononi mwake, akaenda kwao. 15 Nao wakamwambia, Keti sasa, ukalisome masikioni mwetu. Basi, Baruku akalisoma masikioni mwao. 16 Ikawa, walipoyasikia maneno hayo yote, wakatazamana kwa hofu, wakamwambia Baruku, Hatuna budi kumwambia mfalme maneno haya yote. 17 Wakamwuliza Baruku, wakisema, Tuambie sasa; ulipataje kuyaandika maneno haya yote kinywani mwake? 18 Baruku akawajibu, Alinitamkia maneno haya yote kwa kinywa chake, nami nikayaandika kwa wino kitabuni. 19 Ndipo hao wakuu wakamwambia Baruku, Enenda ukajifiche, wewe na Yeremia, wala mtu asipajue mlipo. 20 Wakaenda kwa mfalme uwandani; lakini walikuwa wameliweka lile gombo katika chumba cha Elishama, mwandishi wakayanena maneno hayo yote masikioni mwa mfalme. 21 Basi, mfalme akamtuma Yehudi aende akalilete lile gombo; naye akalitoa katika chumba cha Elishama, mwandishi. Yehudi akalisoma masikioni mwa mfalme, na masikioni mwa wakuu waliosimama mbele ya mfalme. 22 Basi mfalme alikuwa ameketi katika nyumba iliyotumika wakati wa baridi, mwezi wa kenda; na pale palikuwa na moto wa makaa mbele yake. 23 Hata ikawa, Yehudi alipokuwa amekwisha kusoma kurasa tatu nne, mfalme akalikata kwa kijembe, akalitupa katika moto wa makaa, hata gombo lote likawa limekwisha kuteketea katika huo moto wa makaa. 24 Lakini hawakuogopa, wala hawakurarua mavazi yao, wala mfalme, wala watumishi wake hata mmoja waliosikia maneno hayo yote. 25 Hata hivyo Elnathani, na Delaya, na Gemaria, walikuwa wamemsihi mfalme asiliteketeze gombo lile, lakini hakukubali kuwasikia. 26 Mfalme akamwamuru Yerameeli, mwana wa mfalme, na Seraya, mwana wa Azrieli, na Shelemia, mwana wa Abdeeli, wamkamate Baruku, mwandishi, na Yeremia, nabii; lakini Bwana aliwaficha. 27 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia, hapo mfalme alipokuwa amekwisha kuliteketeza gombo lile, na maneno yale aliyoyaandika Baruku, yaliyotoka katika kinywa cha Yeremia, kusema, 28 Haya! Twaa wewe gombo lingine, ukaandike ndani yake maneno yote ya kwanza, yaliyokuwa katika gombo la kwanza, ambalo Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, ameliteketeza. 29 Na katika habari za Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, utasema, Bwana asema hivi, Umeliteketeza gombo hili, ukisema, Mbona umeandika ndani yake, ukisema, Bila shaka mfalme wa Babeli atakuja, na kuiharibu nchi hii, na kukomesha mwanadamu na mnyama pia ndani yake? 30 Basi, Bwana aseme hivi, katika habari za Yehoyakimu, mfalme wa Yuda; Hatakuwa na mtu wa kukaa katika kiti cha enzi cha Daudi; na mzoga wake utatupwa nje wakati wa mchana upigwe kwa hari, na wakati wa usiku upigwe kwa baridi. 31 Nami nitamwadhibu yeye, na wazao wake, na watumishi wake, kwa sababu ya uovu wao, nami nitaleta juu yao, na juu ya wenyeji wa Yerusalemu, na juu ya watu wa Yuda, mabaya yote niliyoyatamka juu yao, lakini hawakukubali kusikiliza. 32 Ndipo Yeremia akatwaa gombo lingine, akampa Baruku, mwandishi, mwana wa Neria, naye akayaandika maneno yote yaliyotoka katika kinywa cha Yeremia, ya kitabu kile alichokiteketeza Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, katika moto; tena maneno mengi zaidi kama yale yakatiwa ndani yake.

Yeremia 37

1 Na Sedekia, mwana wa Yosia, akamiliki badala ya Konia, mwana wa Yehoyakimu, ambaye Nebukadreza amemmilikisha katika nchi ya Yuda. 2 Lakini yeye, wala watumishi wake, wala watu wa nchi, hawakuyasikiliza maneno ya Bwana aliyonena kwa kinywa cha nabii Yeremia. 3 Sedekia, mfalme, akamtuma Yehukali, mwana wa Shelemia, na Sefania, mwana wa Maaseya, kuhani, kwa Yeremia, nabii, kusema, Utuombee sasa kwa Bwana, Mungu wetu. 4 Basi Yeremia alikuwa akiingia na kutoka kati ya watu; kwa maana walikuwa hawakumfunga gerezani. 5 Na jeshi la Farao lilikuwa limetoka nchi ya Misri; na Wakaldayo waliohusuru Yerusalemu, waliposikia habari zao, wakavunja kambi yao mbele ya Yerusalemu. 6 Ndipo neno la Bwana likamjia nabii Yeremia, kusema, 7 Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Mtamwambia hivi mfalme wa Yuda, aliyewatuma kwangu kuniuliza; Angalieni, jeshi la Farao, ambalo linakuja kuwasaidia, litarudi Misri, nchi yao wenyewe. 8 Na Wakaldayo watakuja tena, na kupigana na mji huu; nao watautwaa, na kuuteketeza. 9 Bwana asema hivi, Msijidanganye mkisema, Bila shaka Wakaldayo watatuacha na kwenda zao; maana hawatawaacha. 10 Maana mngelipiga jeshi lote la Wakaldayo wanaopigana nanyi, wakabaki kati yao watu waliojeruhiwa tu, hata hivyo wangeondoka kila mtu katika hema yake, na kuuteketeza mji huu. 11 Hata ikawa, jeshi la Wakaldayo lilipokuwa limevunja kambi yao mbele ya Yerusalemu, kwa kuliogopa jeshi la Farao, 12 ndipo Yeremia akatoka Yerusalemu, ili aende mpaka nchi ya Benyamini, alipokee huko fungu lake kati ya watu. 13 Naye alipokuwa katika lango la Benyamini, akida wa walinzi alikuwapo, jina lake Iriya, mwana wa Shelemia, mwana wa Hanania; akamkamata Yeremia, nabii, akisema, Unakwenda kujiunga na Wakaldayo. 14 Ndipo Yeremia akasema, Ni uongo, siendi kujiunga na Wakaldayo; lakini yeye asimsadiki; basi Iriya akamkamata Yeremia, akamleta kwa wakuu. 15 Nao wakuu wakamkasirikia Yeremia, wakampiga, wakamtia gerezani katika nyumba ya Yonathani, mwandishi; kwa maana ndiyo waliyoifanya kuwa gereza. 16 Basi, Yeremia alipokuwa ameingia katika nyumba ya shimo, na katika vyumba vya ndani; na Yeremia alipokuwa amekaa humo siku nyingi; 17 ndipo Sedekia, mfalme, akatuma watu wamlete; naye mfalme akamwuliza kwa siri ndani ya nyumba yake, akasema, Je! Liko neno lililotoka kwa Bwana? Yeremia akasema, Liko. Akasema pia, Utatiwa katika mikono ya mfalme wa Babeli. 18 Pamoja na haya Yeremia akamwambia mfalme Sedekia, Nimefanya kosa gani juu yako, au juu ya watumishi wako, au juu ya watu hawa, hata mkanitia gerezani? 19 Wako wapi sasa manabii wenu waliowatabiria, wakisema, Mfalme wa Babeli hatakuja juu yenu, wala juu ya nchi hii? 20 Na sasa unisikilize, Ee bwana wangu mfalme; maombi yangu yakapate kibali mbele yako; usinirudishe nyumbani mwa Yonathani, mwandishi, nisije nikafa humo. 21 Ndipo Sedekia mfalme akatoa amri, wakamtia Yeremia katika uwanda wa walinzi; wakampa kila siku mkate mmoja uliotoka katika njia ya waokaji, hata mkate wote wa mji ulipokwisha. Basi Yeremia akakaa katika uwanda wa walinzi.

Yeremia 38

1 Na Shefatia, mwana wa Matani, na Gedalia, mwana wa Pashuri, na Yukali, mwana wa Shelemia, na Pashuri, mwana wa Malkiya, wakayasikia maneno ambayo Yeremia aliwaambia watu wote, kusema, 2 Bwana asema hivi, Akaaye ndani ya mji huu atakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; bali yeye atokaye kwenda kwa Wakaldayo ataishi, naye atapewa maisha yake yawe kama nyara, naye ataishi. 3 Bwana asema hivi, Bila shaka mji huu utatiwa katika mikono ya jeshi la mfalme wa Babeli, naye atautwaa. 4 Ndipo wakuu wakamwambia mfalme, Twakuomba, mtu huyu auawe, kwa kuwa aidhoofisha mikono ya watu wa vita, waliobaki katika mji huu, na mikono ya watu wote, kwa kuwaambia maneno kama hayo; maana mtu huyu hawatafutii watu hawa heri, bali shari. 5 Naye mfalme Sedekia akasema, Tazama, yu mikononi mwenu; maana mfalme siye awezaye kufanya neno lo lote kinyume chenu. 6 Basi wakamtwaa Yeremia, wakamtupa katika shimo la Malkiya, mwana wa mfalme, lililo katika uwanda wa walinzi; wakamshusha kwa kamba. Na mle shimoni hamkuwa na maji, ila matope tu; naye Yeremia akazama katika matope hayo. 7 Basi, Ebedmeleki, Mkushi, towashi, aliyekuwa katika nyumba ya mfalme, aliposikia kama wamemtia Yeremia shimoni; na wakati huo mfalme alikuwa amekaa katika lango la Benyamini; 8 Ebedmeleki akatoka nyumbani mwa mfalme, akamwambia mfalme, akisema, 9 Ee bwana wangu, mfalme, watu hawa wametenda mabaya katika mambo yote waliyomtenda Yeremia, nabii, ambaye wamemtupa shimoni; naye hakosi atakufa pale alipo, kwa sababu ya njaa; kwa kuwa hapana mkate kabisa katika mji. 10 Ndipo mfalme akamwamuru Ebedmeleki, Mkushi, akisema, Chukua pamoja nawe watu thelathini toka hapa, ukamtoe Yeremia shimoni, kabla hajafa. 11 Basi Ebedmeleki akawachukua watu hao pamoja naye, akaingia ndani ya nyumba ya mfalme chini ya ghala, akatoa mle nguo zilizotupwa, na vitambaa vikuukuu, akamtelemshia Yeremia shimoni kwa kamba. 12 Naye Ebedmeleki, Mkushi, akamwambia Yeremia, Tia nguo hizi zilizotupwa, na vitambaa hivi vikuukuu, chini ya kamba kwapani. Naye Yeremia akafanya hivyo. 13 Basi wakamwinua Yeremia kwa kamba hizo, wakamtoa shimoni; naye Yeremia akakaa katika uwanda wa walinzi. 14 Kisha mfalme Sedekia akatuma watu, akamleta nabii Yeremia kwake, ndani ya maingilio ya tatu ya nyumba ya Bwana; mfalme akamwambia Yeremia, Nataka kukuuliza neno, nawe usinifiche neno lo lote. 15 Basi Yeremia akamwambia Sedekia, Kama nikikufunulia neno hilo, je! Hutaniua wewe? Tena, mimi nikikupa shauri wewe hutanisikiliza. 16 Basi Sedekia mfalme akamwapia Yeremia kwa siri, akisema, Kama Bwana aishivyo, yeye aliyetufanyia roho zetu, sitakuua, wala sitakutia katika mikono ya watu hao wanaokutafuta wakuue. 17 Ndipo Yeremia akamwambia Sedekia, Bwana, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kama ukitoka kwenda kwa wakuu wa mfalme wa Babeli, basi nafsi yako utaishi, wala mji huu hautateketezwa; nawe utaishi na nyumba yako; 18 bali ukikataa kutoka kwenda kwa wakuu wa mfalme wa Babeli, basi, mji huu utatiwa katika mikono ya Wakaldayo nao watauteketeza, hata na wewe hutajiepusha na mikono yao. 19 Mfalme Sedekia akamwambia Yeremia, Nawaogopa Wayahudi waliowakimbilia Wakaldayo, wasije wakanitia katika mikono yao, nao wakanidhihaki. 20 Lakini Yeremia akasema, La! Hawatakutoa. Nakusihi, uitii sauti ya Bwana katika hayo ninayokuambia; ndivyo itakavyokufaa, na nafsi yako utaishi. 21 Lakini kama ukikataa kutoka, hili ndilo neno ambalo Bwana amenionyesha; 22 Tazama, wanawake wote, walioachwa ndani ya nyumba ya mfalme wa Yuda, watatolewa na kuchukuliwa kwa wakuu wa mfalme wa Babeli, na wanawake hao watasema, Rafiki zako walio karibu wamekudanganya, nao wamekushinda; na kwa kuwa miguu yako imezama matopeni sasa, wamegeuka na kurudi nyuma. 23 Na watawatoa wake zako, na watoto wako wote, na kuwachukua kwa Wakaldayo; wala wewe hutapona na mikono yao, bali utakamatwa kwa mkono wa mfalme wa Babeli, nawe utakuwa sababu ya kuteketezwa mji huu. 24 Ndipo Sedekia akamwambia Yeremia, Mtu ye yote asipate habari ya maneno haya, nawe hutakufa. 25 Lakini kama wakuu wakisikia ya kuwa nimenena nawe, nao wakija kwako, na kukuambia, Tufunulie sasa uliyomwambia mfalme; usimfiche, nasi hatutakuua; na pia uliyoambiwa na mfalme; 26 basi, utawaambia, Nalimwomba mfalme asinirudishe nyumbani kwa Yonathani, nisije nikafa humo. 27 Ndipo wakuu wakamwendea Yeremia, wakamwuliza; naye akawaambia sawasawa na maneno aliyoamriwa na mfalme. Basi wakaacha kunena naye; maana neno lile halikujulikana. 28 Basi Yeremia akakaa katika uwanda wa walinzi hata siku ile Yerusalemu ulipotwaliwa.

Yeremia 39

1 Hata ikawa, Yerusalemu ulipotwaliwa, (katika mwaka wa kenda wa Sedekia, mfalme wa Yuda, katika mwezi wa kumi, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na jeshi lake lote, wakaja juu ya Yerusalemu, wakauhusuru; 2 katika mwaka wa kumi na mmoja wa Sedekia, mwezi wa nne, siku ya kenda ya mwezi, sehemu ya ukuta wa mji ilibomolewa;) 3 wakuu wote wa mfalme wa Babeli wakaingia, wakaketi katika lango la katikati, yaani, Nergal-Shareza, mnyweshaji, Nebu-Sarseki, mkuu wa matowashi, Nergal-Shareza, mkuu wa wanajimu, pamoja na wakuu wengine wote wa mfalme wa Babeli. 4 Ikawa Sedekia, mfalme wa Yuda, na watu wote wa vita walipowaona, ndipo wakakimbia, wakatoka mjini usiku, kwa njia ya bustani ya mfalme, kwa lango lililokuwa kati ya zile kuta mbili; naye akatoka kwa njia ya Araba. 5 Lakini jeshi la Wakaldayo wakawafuatia, wakampata Sedekia katika nchi tambarare ya Yeriko; nao walipomkamata, wakamleta kwa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, huko Ribla katika nchi ya Hamathi, naye akatoa hukumu juu yake. 6 Ndipo mfalme wa Babeli akawaua wana wa Sedekia huko Ribla mbele ya macho yake; pia mfalme wa Babeli akawaua wakuu wote wa Yuda. 7 Pamoja na hayo akampofusha macho Sedekia, akamfunga kwa pingu ili amchukue mpaka Babeli. 8 Nao Wakaldayo wakaiteketeza nyumba ya mfalme, na nyumba za watu kwa moto, wakazibomoa kuta za Yerusalemu. 9 Basi, Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawachukua mateka mabaki ya watu waliosalia katika mji mpaka Babeli, na hao pia waliouacha mji na kujiunga naye, na mabaki ya watu waliosalia. 10 Lakini Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawaacha baadhi ya maskini wa watu, waliokuwa hawana kitu, katika nchi ya Yuda, akawapa mashamba ya mizabibu na makonde wakati uo huo. 11 Basi Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akamwagiza Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, katika habari za Yeremia, akisema, 12 Mtwae, umtunze sana, wala usimtende neno baya lo lote; lakini umtendee kama atakavyokuambia. 13 Basi Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, na Nebu-Shazbani, mkuu wa matowashi, na Nergal-Shareza, mkuu wa wanajimu, na maakida wakuu wote wa mfalme wa Babeli. 14 wakatuma watu wakamwondoa Yeremia katika uwanda wa walinzi, wakamweka katika mikono ya Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, ili ampeleke nyumbani kwake; basi akakaa pamoja na hao watu. 15 Basi neno la Bwana likamjia Yeremia, wakati ule alipokuwa amefungwa katika uwanda wa walinzi, kusema, 16 Haya! Enenda ukaseme na Ebedmeleki, Mkushi, kusema, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitaupatiliza mji huu maneno yangu kwa mabaya, wala si kwa mema; nayo yatatimizwa mbele yako katika siku hiyo. 17 Lakini nitakuokoa wewe katika siku hiyo, asema Bwana; wala hutatiwa katika mikono ya watu wale unaowaogopa. 18 Kwa maana ni yakini, nitakuokoa, wala hutaanguka kwa upanga, lakini nafsi yako itakuwa kama nyara kwako; kwa kuwa ulinitumaini mimi, asema Bwana.

Yeremia 40

1 Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, baada ya wakati ule Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, alipomwacha aende zake toka Rama, baada ya kumchukua hali ya kufungwa minyororo, pamoja na wafungwa wote wa Yerusalemu na Yuda, waliochukuliwa hali ya kufungwa mpaka Babeli. 2 Naye amiri wa askari walinzi akamtwaa Yeremia, akamwambia, Bwana, Mungu wako, alitamka mabaya haya juu ya mahali hapa; 3 naye Bwana ameyaleta, na kufanya kama alivyosema; kwa sababu mmemwasi Bwana, wala hamkuitii sauti yake; ndiyo maana neno hili limewajia ninyi. 4 Na sasa, tazama, nakufungulia leo minyororo hii iliyo mikononi mwako. Kama ukiona ni vema kwenda Babeli pamoja nami, haya! Njoo, nami nitakutunza sana; lakini kama ukiona ni vibaya kwenda Babeli pamoja nami, basi, acha; tazama, nchi yote i mbele yako; palipo pema machoni pako na pa kukufaa, enenda huko. 5 Alipokuwa bado hajaenda, akasema, Rudi sasa kwa Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, ambaye mfalme wa Babeli amemweka kuwa liwali juu ya miji ya Yuda, ukakae pamoja naye kati ya watu; au enenda po pote utakapoona mwenyewe kuwa pakufaa. Basi, amiri wa askari walinzi akampa vyakula na zawadi, akamwacha aende zake. 6 Basi, Yeremia akaenda kwa Gedalia, mwana wa Ahikamu, huko Mizpa, akakaa pamoja naye kati ya watu wale waliosalia katika nchi. 7 Kisha, wakuu wote wa majeshi waliokuwa katika bara, wao na watu wao, waliposikia kwamba mfalme wa Babeli amemweka Gedalia, mwana wa Ahikamu, kuwa liwali juu ya nchi, na kwamba amemkabidhi wanaume na wanawake na watoto, na baadhi ya maskini wa nchi wasiochukuliwa mateka Babeli; 8 ndipo wakamwendea Gedalia huko Mizpa; nao ni hawa, Ishmaeli, mwana wa Nethania, na Yohana na Yonathani, wana wa Karea, na Seraya, mwana wa Tanhumethi, na wana wa Efai, Mnetofa, na Yezania, mwana wa Mmaaka, wao na watu wao. 9 Na Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, akawaapia wao na watu wao, akisema, Msiogope kuwatumikia Wakaldayo; kaeni katika nchi, mkamtumikie mfalme wa Babeli; nayo itawafaa. 10 Na mimi, tazama, nitakaa Mizpa, ili nisimame mbele ya Wakaldayo watakaotujilia; lakini ninyi chumeni divai, na matunda ya wakati wa jua, na mafuta, mkaviweke vitu hivyo katika vyombo vyenu, mkakae katika miji yenu mliyoitwaa. 11 Kadhalika waliposikia Wayahudi wote, waliokuwa katika Moabu, na kati ya wana wa Amoni, na hao waliokuwa katika Edomu, na hao waliokuwa katika nchi zote, ya kuwa mfalme wa Babeli amewaachia Yuda mabaki, na ya kuwa amemweka Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, juu yao; 12 basi, Wayahudi wote wakarudi kutoka kila mahali walikofukuzwa wakaenda mpaka nchi ya Yuda, wakamwendea Gedalia huko Mizpa, wakakusanya divai, na matunda ya wakati wa jua mengi sana. 13 Tena Yohana, mwana wa Karea, na wakuu wote wa majeshi ya barani, wakamwendea Gedalia huko Mizpa, 14 wakamwambia, Je! Una habari wewe ya kuwa Baalisi, mfalme wa wana wa Amoni, amemtuma Ishmaeli mwana wa Nethania, akuue? Lakini Gedalia, mwana wa Ahikamu, hakusadiki neno hili. 15 Basi, Yohana, mwana wa Karea, akamwambia Gedalia huko Mizpa kwa siri, akisema, Niache niende nikampige Ishmaeli, mwana wa Nethania, wala hapana mtu atakayejua jambo hili; kwani akuue wewe, hata wakatawanyike Wayahudi waliokukusanyikia, na mabaki ya Yuda wakaangamie? 16 Lakini Gedalia, mwana wa Ahikamu, akamwambia Yohana, mwana wa Karea, Usilitende jambo hili, maana unamsingizia Ishmaeli.

Yeremia 41

1 Basi ikawa katika mwezi wa saba, Ishmaeli, mwana wa Nethania, mwana wa Elishama, mmoja wa wazao wa kifalme, tena ni mmoja wa majemadari wa mfalme, na watu kumi pamoja naye, wakamwendea Gedalia, mwana wa Ahikamu, huko Mizpa; nao walikula chakula pamoja huko Mizpa. 2 Akaondoka huyo Ishmaeli, mwana wa Nethania, na watu wale kumi waliokuwa pamoja naye, wakampiga Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, kwa upanga, wakamwua; yeye ambaye mfalme wa Babeli amemweka kuwa liwali wa nchi. 3 Tena Ishmaeli akawaua Wayahudi wote waliokuwa pamoja naye, yaani, pamoja na Gedalia, huko Mizpa, na hao Wakaldayo walioonekana huko, yaani, watu wa vita. 4 Ikawa siku ya pili baada ya kumwua Gedalia, wala hapakuwa na mtu aliyejua habari hii, 5 wakafika watu kadha wa kadha toka Shekemu, na toka Shilo, na toka Samaria, watu themanini, nao wamenyoa ndevu zao, na kurarua nguo zao, nao wamejikata-kata, wakichukua sadaka na ubani mikononi mwao, ili wazilete nyumbani kwa Bwana. 6 Na Ishmaeli, mwana wa Nethania, akatoka Mizpa kwenda kuwalaki, akilia alipokuwa akiendelea; ikawa alipokutana nao akawaambia, Njoni kwa Gedalia, mwana wa Ahikamu. 7 Basi ikawa walipokuwa katikati ya mji, Ishmaeli, mwana wa Nethania, akawaua, akawatupa katika shimo, yeye na watu wale waliokuwa pamoja naye. 8 Lakini watu kumi walionekana miongoni mwao, waliomwambia Ishmaeli, Usituue; kwa maana tuna akiba zetu zilizofichwa kondeni, za ngano, na shayiri, na mafuta, na asali. Basi, akawaacha, asiwaue watu hao pamoja na ndugu zao. 9 Basi, shimo lile, ambalo Ishmaeli ameitupa mizoga ya watu aliowaua, karibu na Gedalia, (ni lile lile alilolichimba Asa, mfalme, kwa kuwa alimwogopa Baasha, mfalme wa Israeli), Ishmaeli, mwana wa Nethania, akalijaza kwa watu wale aliowaua. 10 Kisha Ishmaeli akawachukua mateka watu wote waliosalia, waliokuwa huko Mizpa, yaani, binti za mfalme, na watu wote waliobaki Mizpa, ambao Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, alikuwa amemkabidhi Gedalia, mwana wa Ahikamu; Ishmaeli, mwana wa Nethania, akawachukua mateka. akaondoka, ili awaendee wana wa Amoni. 11 Lakini Yohana, mwana wa Karea, na maakida wote wa majeshi waliokuwa pamoja naye, waliposikia habari za hayo mabaya yote aliyoyatenda Ishmaeli, mwana wa Nethania, 12 wakawatwaa watu wote, wakaenda ili kupigana na Ishmaeli, mwana wa Nethania, nao wakampata karibu na maji makuu ya Gibeoni. 13 Basi, ikawa, watu wote waliokuwa pamoja na Ishmaeli, walipomwona Yohana, mwana wa Karea, na hao maakida wote wa majeshi waliokuwa pamoja naye, ndipo wakafurahi. 14 Basi, watu wote, ambao Ishmaeli amewachukua mateka kutoka Mizpa, wakazunguka, wakarudi, wakamwendea Yohana, mwana wa Karea. 15 Lakini Ishmaeli, mwana wa Nethania, akaokoka pamoja na watu wanane, Yohana asimpate, akawaendea wana wa Amoni. 16 Ndipo Yohana, mwana wa Karea, na maakida wote wa majeshi waliokuwa pamoja naye, wakawatwaa hao watu wote waliosalia, aliowapata tena katika mikono ya Ishmaeli, mwana wa Nethania, huko Mizpa, baada ya kumwua Gedalia, mwana wa Ahikamu, yaani, watu wa vita, na wanawake na watoto, na matowashi, aliowarudisha toka Gibeoni; 17 wakaenda zao, wakakaa katika Geruthi Kimhamu, ulio karibu na Bethlehemu, ili wapate kuingia Misri, 18 kwa sababu ya Wakaldayo; maana waliwaogopa, kwa sababu Ishmaeli, mwana wa Nethania, amemwua Gedalia, mwana wa Ahikamu, ambaye mfalme wa Babeli amemweka kuwa liwali juu ya nchi.

Yeremia 42

1 Ndipo maakida wote wa majeshi, na Yohana, mwana wa Karea, na Yezania, mwana wa Hoshaya, na watu wote tangu wadogo hata wakubwa, wakakaribia, 2 wakamwambia Yeremia, nabii, Twakusihi, maombi yetu yakubaliwe mbele yako, ukatuombee kwa Bwana, Mungu wako, yaani, watu hawa wote waliosalia; maana tumesalia wachache tu katika watu wengi, kama macho yako yatuonavyo; 3 ili kwamba Bwana, Mungu wako, atuonyeshe njia ambayo yatupasa tuiendee, na jambo litupasalo tulitende. 4 Ndipo Yeremia, nabii, akawaambia, Nimewasikia; tazama, nitamwomba Bwana, Mungu wenu, sawasawa na maneno yenu; tena itakuwa, neno lo lote ambalo Bwana atawajibu, nitawaambia; sitawazuilia neno liwalo lote. 5 Wakamwambia Yeremia, Bwana na awe shahidi wa kweli na uaminifu kati yetu; ikiwa hatufanyi sawasawa na neno lile, ambalo Bwana, Mungu wako, atakutuma utuletee. 6 Likiwa jema, au likiwa baya, sisi tutaitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, ambaye tunakutuma kwake; ipate kuwa faida yetu, tunapoitii sauti ya Bwana, Mungu wetu. 7 Ikawa, baada ya siku kumi, neno la Bwana likamjia Yeremia. 8 Ndipo akamwita Yohana, mwana wa Karea, na maakida wote wa majeshi waliokuwa pamoja naye, na watu wote tangu wadogo hata wakubwa, 9 akawaambia, Bwana, Mungu wa Israeli, ambaye mlinituma kwake, ili niyaweke maombi yenu mbele yake, asema hivi; 10 Ikiwa mtakaa bado katika nchi hii, ndipo nitawajenga, wala sitawabomoa, nami nitawapanda, wala sitawang'oa; kwa maana nayajutia mabaya niliyowatenda. 11 Msimwogope mfalme wa Babeli, mnayemwogopa; msimwogope, asema Bwana; maana mimi ni pamoja nanyi, niwaokoe, na kuwaponya na mkono wake. 12 Nami nitawapa rehema, kwamba awarehemu ninyi, na kuwarudisha mkae katika nchi yenu wenyewe. 13 Lakini mkisema, Hatutaki kukaa katika nchi hii; msiitii sauti ya Bwana, Mungu wenu; 14 mkisema, La! Lakini tutakwenda nchi ya Misri, ambayo hatutaona vita, wala kuisikia sauti ya tarumbeta, wala kuona njaa kwa kukosa chakula; nasi tutakaa huko; 15 basi, lisikieni neno la Bwana, enyi mabaki ya Yuda; Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ikiwa mwakaza nyuso zenu kuingia Misri, na kwenda kukaa huko; 16 basi, itakuwa, upanga mnaouogopa utawapata huko, katika nchi ya Misri, nayo njaa mnayoiogopa itawafuatia mbio huko Misri, nanyi mtakufa huko. 17 Haya ndiyo yatakayowapata watu wote waelekezao nyuso zao kwenda Misri, na kukaa huko; watakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; hapana mtu awaye yote miongoni mwao atakayesalia, au kuokoka katika mabaya nitakayoyaleta juu yao. 18 Maana Bwana wa majeshi Mungu wa Israeli, asema hivi, Kama hasira yangu, na ghadhabu yangu, ilivyomwagwa juu ya hao wakaao Yerusalemu, ndivyo ghadhabu yangu itakavyomwagwa juu yenu, mtakapoingia Misri; nanyi mtakuwa apizo, na ajabu, na laana, na aibu; wala hamtapaona mahali hapa tena. 19 Bwana asema katika habari zenu, enyi mabaki ya Yuda, Msiingie Misri; jueni sana ya kuwa nimewashuhudia hivi leo. 20 Maana mmetenda kwa hila juu ya nafsi zenu wenyewe; kwa kuwa mmenituma kwa Bwana, Mungu wenu, mkisema, Utuombee kwa Bwana, Mungu wetu, ukatufunulie sawasawa na yote atakayoyanena Bwana, Mungu wetu, nasi tutayatenda; 21 nami nimewafunulia haya leo; lakini ninyi hamkuitii sauti ya Bwana, Mungu wenu, katika neno lo lote ambalo amenituma kwenu. 22 Basi, sasa jueni sana ya kuwa mtakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni, katika mahali pale mnapopatamani kwenda na kukaa.

Yeremia 43

1 Ikawa Yeremia alipokwisha kuwaambia watu wote maneno yote ya Bwana, Mungu wao, ambayo Bwana, Mungu wao, amemtuma kwao, yaani, maneno hayo yote, 2 ndipo Azaria, mwana wa Hoshaya, na Yohana mwana wa Karea, na watu wote wenye kiburi wakanena, wakimwambia Yeremia, Unasema uongo; Bwana, Mungu wetu, hakukutuma useme, Msiende Misri kukaa huko; 3 bali Baruku, mwana wa Neria, akushawishi kinyume chetu, ili kututia katika mikono ya Wakaldayo, ili watuue, na kutuchukua mateka mpaka Babeli. 4 Basi Yohana, mwana wa Karea, na wakuu wote wa majeshi, na watu wote hawakuitii sauti ya Bwana, kwamba wakae katika nchi ya Yuda. 5 Lakini Yohana, mwana wa Karea, na wakuu wote wa majeshi, wakawatwaa wote waliosalia wa Yuda, waliokuwa wamerudi kutoka taifa zote walikofukuzwa, wakae katika Yuda; 6 wanaume, na wanawake, na watoto, na binti za mfalme, na kila mtu ambaye Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, amemwacha pamoja na Gedalia, mwana wa Ahikamu, mwana wa Shafani, pia na Yeremia, nabii, na Baruku, mwana wa Neria; 7 wakaingia nchi ya Misri; maana hawakuitii sauti ya Bwana; wakafika hata Tahpanesi. 8 Ndipo neno la Bwana likamjia Yeremia huko Tahpenesi, kusema, 9 Twaa mawe makubwa mikononi mwako, ukayafiche ndani ya chokaa ya kazi ya matofali, penye maingilio ya nyumba ya Farao huko Tahpanesi, machoni pa watu wa Yuda; 10 ukawaambie, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitatuma na kumtwaa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mtumishi wangu, nami nitaweka kiti chake cha enzi juu ya mawe haya niliyoyaficha; naye atatandaza hema yake ya fahari juu yake. 11 Naye atakuja, na kuipiga nchi ya Misri; watu walioandikiwa kufa watakufa, nao walioandikiwa kuwa mateka watakuwa mateka, nao walioandikiwa kupigwa kwa upanga watapigwa kwa upanga. 12 Nami nitawasha moto katika nyumba za miungu ya Misri, na kuziteketeza, na kuwachukua mateka; naye atajipamba kwa nchi ya Misri, kama vile mchungaji avaavyo nguo zake; naye atatoka huko na amani. 13 Naye atazivunja nguzo za Bethshemeshi, iliyoko huko katika nchi ya Misri, na nyumba za miungu ya Misri ataziteketeza.

Yeremia 44

1 Neno lililomjia Yeremia, katika habari za Wayahudi wote waliokaa katika nchi ya Misri, waliokaa Migdoli, na Tahpanesi, na Nofu, na katika nchi ya Pathrosi, kusema, 2 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ninyi mmeona mabaya yote niliyoleta juu ya Yerusalemu, na juu ya miji yote ya Yuda; na, tazama, ni ukiwa leo, wala hapana mtu akaaye ndani yake; 3 kwa sababu ya uovu wao, waliotenda ili kunikasirisha, kwa kuwa walikwenda kufukiza uvumba, na kuwatumikia miungu mingine, ambao hawakuwajua, wao, wala ninyi, wala baba zenu. 4 Tena nalituma kwenu watumishi wangu wote, manabii, nikiamka mapema na kuwatuma, nikisema, Basi ninyi; msilifanye chukizo hili linichukizalo. 5 Lakini hawakusikiliza, wala hawakutega masikio yao, ili wageuke na kuacha uovu wao, wasifukizie uvumba miungu mingine. 6 Kwa sababu hiyo ghadhabu yangu, na hasira yangu, zilimwagika, nazo ziliwaka katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, na miji hiyo imeachwa ukiwa, na kuharibika, kama ilivyo leo. 7 Basi, sasa, Bwana, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa nini mnafanya uovu huu mkubwa juu ya nafsi zenu wenyewe, kujikatilia mbali mwanamume na mwanamke, mtoto mchanga na anyonyaye, mtoke kati ya Yuda, msijiachie mtu abakiye; 8 kwa kuwa mnanikasirisha kwa matendo ya mikono yenu, mkifukizia uvumba miungu mingine katika nchi ya Misri, mlikokwenda kukaa ugenini; mpate kukatiliwa mbali, na kuwa laana, na aibu, katika mataifa yote ya dunia? 9 Je! Mmeusahau uovu wa baba zenu, na uovu wa wafalme wa Yuda, na uovu wa wake zao, na uovu wenu wenyewe, na uovu wa wake zenu, walioutenda katika nchi ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu? 10 Hawajanyenyekea hata leo, wala hawakuogopa, wala hawakuenenda katika sheria yangu, wala katika amri zangu, nilizoweka mbele yenu, na mbele ya baba zenu. 11 Basi, kwa sababu hiyo Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitaelekeza uso wangu juu yenu, ili niwaletee mabaya, hata kukatilia mbali Yuda yote. 12 Nami nitawatwaa mabaki ya Yuda, walioelekeza nyuso zao kuiingia nchi ya Misri, wakae huko, nao wataangamia wote pia; wataanguka katika nchi ya Misri; wataangamia kwa upanga, na kwa njaa; watakufa, tangu wadogo hata wakubwa, kwa upanga, na kwa njaa; nao watakuwa apizo, na ajabu, na laana, na aibu. 13 Kwa maana nitawaadhibu wakaao katika nchi ya Misri, kama nilivyouadhibu Yerusalemu, kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; 14 hata katika watu wale wa Yuda waliosalia, waliokwenda nchi ya Misri ili wakae huko, hapatakuwa na mtu ye yote atakayepona, wala atakayesalia, na kupata kurudi nchi ya Yuda, ambayo wanatamani kurudi ili kukaa huko; maana hapana atakayerudi, ila wao watakaopona. 15 Ndipo watu wote waliojua ya kuwa wake zao waliwafukizia uvumba miungu mingine, na wanawake wote waliosimama karibu, mkutano mkubwa, yaani, watu wote waliokaa katika nchi ya Misri, katika Pathrosi, wakamjibu Yeremia, wakisema, 16 Neno lile ulilotuambia kwa jina la Bwana, sisi hatutakusikiliza. 17 Lakini bila shaka tutalitimiza kila neno lililotoka katika vinywa vyetu, kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, kama tulivyotenda sisi, na baba zetu, na wafalme wetu, na wakuu wetu, katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu; maana wakati huo tulikuwa na chakula tele, na kufanikiwa, wala hatukuona mabaya. 18 Lakini tulipoacha kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, tumepungukiwa na vitu vyote; na kuangamizwa kwa upanga, na kwa njaa. 19 Nasi tulipomfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, je! Tulimfanyizia mikate, ili kumwabudu, na kummiminia mamiminiko, waume zetu wasipokuwapo? 20 Ndipo Yeremia akawaambia watu wote, wanaume na wanawake, yaani, watu wote waliompa jibu lile, akisema, 21 Uvumba mliofukiza katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, ninyi, na baba zenu, wafalme wenu, na wakuu wenu, na watu wa nchi, je! Bwana hakuwakumbuka watu hao? Je! Jambo hili halikuingia moyoni mwake? 22 Hata Bwana asiweze kuvumilia tena, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu, na kwa sababu ya machukizo mliyoyafanya; kwa sababu hiyo nchi yenu imekuwa ukiwa, na ajabu, na laana, isikaliwe na mtu kama ilivyo leo. 23 Kwa sababu mmefukiza uvumba, na kwa sababu mmetenda dhambi juu ya Bwana, wala hamkuitii sauti ya Bwana, wala hamkwenda katika torati yake, wala katika amri zake, wala katika shuhuda yake; ndiyo maana mabaya haya yamewapata kama ilivyo leo. 24 Tena Yeremia akawaambia watu wote, na wanawake wote, Lisikieni neno hili la Bwana, ninyi nyote wa Yuda, mliopo hapa katika nchi ya Misri; 25 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ninyi na wake zenu mmenena kwa vinywa vyenu, na kutimiza kwa mikono yenu, mkisema, Bila shaka tutazitimiza nadhiri zetu tulizoziweka, na kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji; basi, zithibitisheni nadhiri zenu, zitimizeni nadhiri zenu. 26 Basi, kwa sababu hiyo lisikieni neno la Bwana, ninyi nyote wa Yuda, mnaokaa katika nchi ya Misri, Tazama, nimeapa kwa jina langu kuu, asema Bwana, ya kwamba jina langu halitatajwa tena katika kinywa cha mtu awaye yote wa Yuda, katika nchi yote ya Misri, akisema, Kama Bwana MUNGU aishivyo! 27 Tazama, nawaangalia niwaletee mabaya, wala si mema; nao watu wote wa Yuda, waliopo hapa katika nchi ya Misri, wataangamizwa kwa upanga, na kwa njaa, hata wakomeshwe kabisa. 28 Nao watakaoukimbia upanga, watatoka katika nchi ya Misri, na kuiingia nchi ya Yuda, watu wachache sana; na wote wa Yuda waliosalia, waliokwenda nchi ya Misri ili kukaa huko, watajua ni neno la nani litakalosimama, neno langu, au neno lao. 29 Na hii ndiyo itakayokuwa ishara kwenu, asema Bwana, kwamba mimi nitawaadhibu ninyi mahali hapa, mpate kujua ya kuwa maneno yangu yatasimama juu yenu, kuwaletea mabaya bila shaka; 30 Bwana asema hivi, Tazama, nitamtia Farao Hofra, mfalme wa Misri, katika mikono ya adui zake, na katika mikono yao wamtafutao roho yake; kama vile nilivyomtia Sedekia, mfalme wa Yuda, katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, adui yake aliyemtafuta roho yake.

Yeremia 45

1 Neno hili ndilo ambalo Yeremia, nabii, alimwambia Baruku, mwana wa Neria, alipoyaandika maneno haya katika kitabu kwa kinywa cha Yeremia, mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, kusema, 2 Bwana, Mungu wa Israeli, akuambia wewe Ee Baruku; 3 Ulisema, Ole wangu! Kwa maana Bwana ameongeza huzuni pamoja na maumivu yangu. Nimechoka kwa ajili ya kuugua kwangu, wala sioni raha. 4 Basi, mwambie hivi, Bwana asema hivi, Tazama, niliyoyajenga nitayabomoa, na niliyoyapanda nitayang'oa; na haya yatakuwa katika nchi yote. 5 Je! Unajitafutia mambo makuu? Usiyatafute; kwa maana tazama, nitaleta mabaya juu ya wote wenye mwili, asema Bwana; lakini roho yako nitakupa iwe nyara, katika mahali pote utakapokwenda.

Yeremia 46

1 Neno la Bwana lililomjia Yeremia, nabii, katika habari za mataifa. 2 Katika habari za Misri; habari za jeshi la Farao Neko, mfalme wa Misri, lililokuwa karibu na mto Frati katika Karkemishi, ambalo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alilipiga katika mwaka wa nne wa Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda. 3 Tengenezeni kigao na ngao, mkakaribie ili kupigana. 4 Watandikeni farasi; pandeni, enyi mpandao farasi; simameni na chapeo zenu, isugueni mikuki; zivaeni dirii. 5 Nimeyaona haya kwa sababu gani? Wamefadhaika, wamerudi nyuma; mashujaa wao wamevunjika-vunjika; wanakimbia upesi sana, hawatazami nyuma; hofu ziko pande zote; asema Bwana. 6 Mtu mwepesi asikimbie, wala shujaa asiokoke; pande za kaskazini karibu na mto Frati wamejikwaa na kuanguka. 7 Nani huyu ajiinuaye kama mto Nile, Ambaye maji yake yanajirusha kama mito? 8 Misri anajiinua kama mto Nile, Na maji yake yanajirusha kama mito; Asema, Nitajiinua, nitaifunikiza nchi; Nitauharibu mji na hao wakaao ndani yake. 9 Haya! Pandeni, enyi farasi; Jihimizeni, enyi magari ya vita; Mashujaa nao na watoke nje Kushi na Puti, watumiao ngao; Nao Waludi, washikao uta na kuupeta. 10 Maana hiyo ni siku ya Bwana, Bwana wa majeshi, Siku ya kisasi, ili ajilipize kisasi juu ya adui zake; Nao upanga utakula na kushiba, Utakunywa damu yao hata kukinai; Maana Bwana, Bwana wa majeshi, ana sadaka yake Katika nchi ya kaskazini karibu na mto Frati. 11 Panda uende Gileadi, ukatwae zeri, Ee binti, bikira wa Misri; unatumia dawa nyingi bure tu; hupati kupona kamwe. 12 Mataifa wamesikia habari za aibu yako, nayo dunia imejaa kilio chako; maana shujaa amejikwaa juu ya shujaa mwenzake, wameanguka wote wawili pamoja. 13 Neno hili ndilo ambalo Bwana alimwambia Yeremia, nabii, kueleza jinsi Nebukadreza, mfalme wa Babeli, atakavyokuja na kuipiga nchi ya Misri. 14 Tangazeni habari hii katika Misri, mkaihubiri katika Migdoli, na kuihubiri katika Nofu, na Tahpanesi; semeni, Simama, ujifanye tayari kwa maana upanga umekula pande zako zote. 15 Mbona mashujaa wako wamechukuliwa mbali? Hawakusimama kwa sababu Bwana aliwafukuza. 16 Aliwakwaza wengi, naam, wakaangukiana wao kwa wao; wakasema, Haya! Na tuondoke, tukarudi kwa watu wetu wenyewe, hata nchi tuliyozaliwa, tuukimbie upanga unaotuonea. 17 Wakalia huko, Farao, mfalme wa Misri, ni kishindo tu; muhula alioandikiwa ameuacha upite. 18 Kama mimi niishivyo, asema Mfalme, ambaye jina lake ni Bwana wa majeshi, hakika yake, kama Tabori katika milima, na kama Karmeli karibu na bahari, ndivyo atakavyokuja. 19 Ee binti ukaaye katika Misri, Ujiweke tayari kwenda zako hali ya kufungwa; Kwa maana Nofu utakuwa ukiwa, Utateketezwa, usikaliwe na watu. 20 Misri ni mtamba mzuri sana, lakini uharibifu umekuja, Umekuja utokao pande za kaskazini. 21 Na watu wake waliojiwa, walio kati yake, Ni kama ndama waliowanda malishoni; Maana wao nao wamerudi nyuma, Wamekimbia wote pamoja, wasisimame; Maana siku ya msiba wao imewafikilia, Wakati wa kujiliwa kwao. 22 Sauti yake ni kama nyoka, wajapo kwa nguvu, Watamjia na mashoka, kama wachanja kuni. 23 Wataukata msitu wake, asema Bwana, ingawa haupenyeki; Kwa maana ni wengi kuliko nzige, hawahesabiki. 24 Binti ya Misri ataaibishwa; Atatiwa mikononi mwa watu wa kaskazini. 25 Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, nitamwadhibu Amoni wa No, na Farao, na Misri, pamoja na miungu yake, na wafalme wake, naam, Farao, na hao wanaomtumainia; 26 nami nitawatia katika mikono ya hao wanaowatafuta roho zao, na katika mikono ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, na katika mikono ya watumishi wake; na baada ya hayo itakaliwa na watu, kama katika siku za kale, asema Bwana. 27 Lakini usiogope wewe, Ee Yakobo, mtumishi wangu; wala usifadhaike, Ee Israeli; kwa maana, tazama, nitakuokoa toka mbali, na wazao wako toka nchi ya uhamisho wao; na Yakobo atarudi, naye atatulia na kustarehe, wala hapana mtu atakayemtia hofu. 28 Usiogope wewe, Ee Yakobo, mtumishi wangu, asema Bwana; kwa maana mimi ni pamoja nawe; maana nitawakomesha kabisa mataifa yote huko nilikokufukuza, bali sitakukomesha wewe kabisa; lakini nitakurudi kwa hukumu, wala sitakuacha bila adhabu.

Yeremia 47

1 Neno la Bwana lililomjia Yeremia, nabii, katika habari za Wafilisti, kabla Farao hajapiga Gaza. 2 Bwana asema hivi, Tazama, maji yanatokea katika pande za kaskazini, nayo yatakuwa mto ufurikao, nayo yataifunika nchi, na kila kitu kilichomo, huo mji na wote wakaao ndani yake; nao watu watalia na watu wote wakaao katika nchi watapiga yowe. 3 Kwa sababu ya mshindo wa kukanyaga kwato za farasi wake walio hodari, kwa sababu ya mwendo wa mbiombio wa magari yake ya vita; kwa sababu ya ngurumo ya magurudumu yake, hao akina baba hawatazami nyuma ili kuwaangalia watoto wao, kwa kuwa mikono yao ni dhaifu; 4 kwa sababu ya siku ijayo kuwaangamiza Wafilisti wote, kukatilia mbali kila msaidizi wa Tiro na Sidoni asaliaye; maana Bwana atawaharibu Wafilisti, mabaki ya kisiwa cha Kaftori. 5 Upaa umeupata Gaza; Ashkeloni umenyamazishwa Mabaki ya bonde lao; Hata lini utajikata-kata? 6 Ee upanga wa Bwana, Siku ngapi zitapita kabla hujatulia? Ujitie katika ala yako; Pumzika, utulie. 7 Utawezaje kutulia, Ikiwa Bwana amekupa agizo? Juu ya Ashkeloni na juu ya pwani, Ndipo alipoyaamuru hayo.

Yeremia 48

1 Habari za Moabu. Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Ole wake Nebo! Kwa maana umeharibika; Kiriathaimu umeaibishwa, umetwaliwa; Misgabu umeaibishwa, nao umebomolewa. 2 Sifa za Moabu haziko tena; katika Heshboni wameazimia mabaya juu yake, Haya! Njoni, na tumkatilie mbali asiwe taifa. Wewe nawe, Ee Madmena, utanyamazishwa; upanga utakufuatia. 3 Sauti ya kilio toka Horonaimu, Ya kutekwa na uharibifu mkuu. 4 Moabu umeharibika; Wadogo wake wamewasikiza watu kilio. 5 Kwa maana watu wapandapo huko Luhithi Watapanda wasiache kulia; Nao watu watelemkapo huko Horonaimu Wameisikia huzuni ya kilio cha uharibifu. 6 Haya! Kimbieni! Jiokoeni nafsi zenu! Mkawe kama mtu aliye mkiwa. 7 Maana, kwa kuwa umeyatumainia matendo yako, na hazina zako, wewe nawe utatwaliwa; na Kemoshi atatoka aende katika uhamisho, makuhani wake na wakuu wake pamoja. 8 Naye mwenye kuteka nyara atakuja juu ya kila mji, wala hapana mji utakaookoka; bonde nalo litaangamia, nayo nchi tambarare itaharibiwa; kama Bwana alivyosema. 9 Mpe Moabu mabawa, apate kuruka na kwenda zake; na miji yake itakuwa ukiwa, isiwe na mtu wa kukaa ndani yake. 10 Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya Bwana kwa ulegevu; na alaaniwe auzuiaye upanga wake usimwage damu. 11 Moabu amestarehe tangu ujana wake, naye ametulia juu ya sira zake, wala hakumiminwa kutoka chombo kimoja kutiwa chombo kingine, wala hakwenda kufungwa; kwa hiyo ladha yake anakaa nayo, wala harufu yake haikubadilika. 12 Basi, tazama, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo nitampelekea wamiminao, nao watammimina, nao watamwaga vyote vilivyomo vyomboni mwake, na kuzivunja chupa zake vipande vipande. 13 Na Moabu ataona haya kwa ajili ya Kemoshi, kama nyumba ya Israeli ilivyoona haya kwa ajili ya Betheli, matumaini yao. 14 Mwasemaje ninyi, Sisi tu mashujaa, watu hodari wa vita. 15 Moabu ameharibika, na moshi wa miji yake umepanda; na vijana wake wateule wametelemka kwenda kuchinjwa, asema Mfalme, ambaye jina lake ni Bwana wa majeshi. 16 Msiba wa Moabu umefika karibu, Na mateso yake yanafanya haraka. 17 Ninyi nyote mnaomzunguka, mlilieni, Nanyi nyote mlijuao jina lake, semeni, Jinsi ilivyovunjika fimbo ya enzi, Fimbo ile iliyokuwa nzuri! 18 Ee binti ukaaye Diboni, Shuka toka utukufu wako, ukae katika kiu; Maana atekaye Moabu amepanda juu yako, Ameziharibu ngome zako. 19 Wewe ukaaye Aroeri, Simama kando ya njia upeleleze; Mwulize mwanamume akimbiaye na mwanamke atorokaye, Sema, Imetendeka nini? 20 Moabu ameaibishwa, kwa maana amevunjika; Pigeni yowe na kulia; Tangazeni habari hii katika Arnoni, Ya kuwa Moabu ameharibika. 21 Na hukumu imeifikilia nchi tambarare; juu ya Holoni, na juu ya Yasa, na juu ya Mefaathi; 22 na juu ya Diboni, na juu ya Nebo, na juu ya Beth-diblathaimu; 23 na juu ya Kiriathaimu, na juu ya Beth-gamuli, na juu ya Beth-meoni; 24 na juu ya Keriothi, na juu ya Bozra, na juu ya miji yote ya nchi ya Moabu, iliyo mbali na iliyo karibu. 25 Pembe ya Moabu imekatika, na mkono wake umevunjika, asema Bwana. Mlevyeni; kwa maana alijitukuza juu ya Bwana 26 na Moabu atagaa-gaa katika matapiko yake, naye atadhihakiwa. Kwa maana Israeli, je! Hakuwa dhihaka kwako? 27 Alionekana kati ya wevi? Maana kila umtajapo watikisa kichwa chako. 28 Enyi mkaao Moabu, iacheni miji, Enendeni kukaa majabalini; Mkawe kama njiwa afanyaye kioto chake Katika ubavu wa mdomo wa shimo. 29 Tumesikia habari za kiburi cha Moabu; Ya kuwa ana kiburi kingi; Jeuri yake, na kiburi chake, na majivuno yake, Na jinsi alivyotakabari moyoni mwake. 30 Najua ghadhabu yake, asema Bwana, ya kuwa si kitu; majisifu yake hayakutenda neno lo lote. 31 Kwa sababu hiyo nitampigia yowe Moabu, naam, nitapiga kelele kwa ajili ya Moabu yote; nitawaombolezea watu wa Kir-heresi. 32 Nitakulilia, Ee mzabibu wa Sibma, kwa vilio vipitavyo vilio vya Yazeri; matawi yako yalipita juu ya bahari, yalifika hata bahari ya Yazeri; atekaye nyara ameyaangukia matunda yako ya wakati wa jua, na mavuno yako ya zabibu. 33 Furaha na shangwe zimeondoshwa, katika shamba lizaalo sana, na katika nchi ya Moabu; nami nimeikomesha divai katika mashinikizo; hapana mtu atakayekanyaga zabibu kwa shangwe; shangwe ile itakuwa si shangwe. 34 Toka kilio cha Heshboni mpaka Eleale, naam, mpaka Yahasa, wametoa sauti zao, toka Soari mpaka Horonaimu, hata Eglath-shelishia; maana maji ya Nimrimu nayo yatakuwa ukiwa. 35 Pamoja na hayo, asema Bwana, nitamkomesha katika Moabu mtu atoaye sadaka katika mahali pa juu, naye awafukiziaye uvumba miungu yake. 36 Kwa sababu hiyo moyo wangu watoa sauti kama filimbi kwa ajili ya Moabu, na kwa ajili ya watu wa Kir-heresi, moyo wangu watoa sauti kama filimbi; kwa kuwa wingi aliojipatia umepotea. 37 Maana kila kichwa kina upaa, na ndevu zote zimenyolewa; mikono yote ina alama za chale, na viuno vyote vimevikwa nguo za magunia. 38 Juu ya dari zote za nyumba za Moabu, na katika njia kuu zake, pana maombolezo, kila mahali; kwa maana nimevunja Moabu kama chombo kisichopendeza, asema Bwana. 39 Jinsi alivyovunjika! Pigeni yowe! Jinsi Moabu alivyogeuza kisogo kwa haya! Hivyo ndivyo Moabu atakavyokuwa dhihaka, na sababu ya kuwashangaza watu wote wamzungukao. 40 Maana Bwana asema hivi, Tazama, ataruka kama tai, na kutandaza mabawa yake juu ya Moabu. 41 Miji imetwaliwa, ngome zimeshambuliwa, na mioyo ya mashujaa wa Moabu siku hiyo itakuwa kama moyo wa mwanamke katika utungu wake. 42 Na Moabu ataangamizwa, asiwe taifa tena, kwa sababu alijitukuza juu ya Bwana. 43 Hofu, na shimo, na mtego, zaja juu yako, Ee mwenyeji wa Moabu, asema Bwana. 44 Aikimbiaye hofu ataanguka shimoni; na yeye atokaye shimoni atanaswa kwa mtego; maana nitaleta juu yake, yaani, juu ya Moabu, mwaka wa kujiliwa kwake, asema Bwana. 45 Wamekimbia, wasio na nguvu Wanasimama chini ya kivuli cha Heshboni; Ila moto umetoka katika Heshboni, Na mwali wa moto toka kati ya Sihoni Nao umekula pembe ya Moabu, Na utosi wa kichwa wa watu wapigao kelele. 46 Ole wako! Ee Moabu, Watu wa Kemoshi wamepotea; Maana wana wako wamechukuliwa mateka, Na binti zako wamekwenda utumwani. 47 Lakini nitawarudisha watu wa Moabu walio utumwani, siku za mwisho, asema Bwana. Hukumu ya Moabu imefikilia hapa.

Yeremia 49

1 Habari za wana wa Amoni. Bwana asema hivi, Je, Israeli hana wana? Je! Hana mrithi? Basi, mbona Malkamu anamiliki Gadi, na watu wake wanakaa katika miji yake? 2 Basi, kwa sababu hiyo, tazama, siku zinakuja, asema Bwana, nitakaposikizisha mshindo wa vita juu ya Raba, mji wa Amoni, nao utakuwa magofu ya ukiwa, na binti zake watateketezwa kwa moto; ndipo Israeli watawamiliki wao waliokuwa wakimmiliki, asema Bwana. 3 Piga yowe, Ee Heshboni, Kwa maana Ai umeangamizwa; Lieni, enyi binti za Raba, Mjivike nguo za magunia; Ombolezeni, mkipiga mbio Huko na huko kati ya maboma; Maana Malkamu atakwenda kuhamishwa, Makuhani wake na wakuu wake pamoja. 4 Mbona unajisifu kwa sababu ya mabonde, bonde lako litiririkalo, Ee binti mwenye kuasi? Utumainiaye hazina zako, ukisema, Ni nani atakayenijilia? 5 Tazama, nitaleta hofu juu yako, asema Bwana, Bwana wa majeshi, itakayotoka kwa wote wakuzungukao; nanyi mtafukuzwa nje, kila mtu mbali kabisa, wala hapana mtu wa kuwakusanya wapoteao. 6 Lakini baada ya hayo nitawarudisha wana wa Amoni walio utumwani, asema Bwana. 7 Habari za Edomu. Bwana wa majeshi asema hivi, Je! Hapana tena hekima katika Temani? Mashauri yamewapotea wenye busara? Je! Imetoweka hekima yao? 8 Kimbieni, rudini nyuma, kaeni chini sana, enyi mnaokaa Dedani; maana nitaleta msiba wa Esau juu yake, wakati nitakapomwangalia. 9 Je! Kama wachuma zabibu wangekujia, wasingeacha zabibu ziokotwe? Kama wangekujia wevi usiku, wasingeharibu hata watakapopata vya kutosha? 10 Lakini nimemwacha Esau hana kitu, nimepafunua mahali pake pa siri, wala hataweza kujificha; kizazi chake kimeangamizwa, na ndugu zake, na jirani zake, naye mwenyewe hayuko. 11 Waache watoto wako wasio na baba, mimi nitawahifadhi hai, na wajane wako na wanitumaini mimi. 12 Maana Bwana asema hivi, Tazama, wale wasioandikiwa kunywea kikombe, watakinywea, ni hakika; na wewe je! U mtu ambaye hataadhibiwa kabisa? Hukosi utaadhibiwa, naam, kunywa utakunywa. 13 Kwa maana nimeapa kwa nafsi yangu, asema Bwana, kwamba Bozra utakuwa ajabu, na aibu, na ukiwa, na laana; na miji yake yote itakuwa ukiwa wa daima. 14 Nimepata habari kwa Bwana, Na mjumbe ametumwa kati ya mataifa, Akisema, Jikusanyeni, mkaujie, Mkainuke kwenda vitani. 15 Maana nimekufanya mdogo kati ya mataifa, Na kudharauliwa katika watu. 16 Katika habari za kuogofya kwako, Kiburi cha moyo wako kimekudanganya, Wewe ukaaye katika pango za majabali, Ushikaye kilele cha milima; Ujapofanya kioto chako juu sana kama tai, Nitakushusha kutoka huko; asema Bwana. 17 Na Edomu atakuwa ajabu; kila mtu apitaye atashangaa, na kuzomea, kwa sababu ya mapigo yake yote. 18 Kama vile vilivyotokea wakati wa kuangushwa Sodoma na Gomora, na miji iliyokuwa karibu nayo, asema Bwana; hapana mtu atakayekaa huko, wala hapana mwanadamu atakayekaa huko kama mgeni akaavyo. 19 Angalia, atapanda kama simba toka kiburi cha Yordani juu ya malisho yasiyonyauka; lakini nitamkimbiza ghafula ayaache; na yeye aliye mteule nitamweka juu yake; maana ni nani aliye kama mimi? Tena ni nani atakayeniandikia muda? Tena ni mchungaji yupi atakayesimama mbele zangu? 20 Basi, lisikieni shauri la Bwana; Alilolifanya juu ya Edomu; Na makusudi yake aliyoyakusudia Juu yao wakaao Temani; Hakika watawaburura, naam, wadogo wa kundi; Hakika malisho yao yatafadhaika kwa ajili yao. 21 Nchi yatetemeka kwa sauti ya kuanguka kwao; Kuna kilio, sauti yake yasikiwa katika Bahari ya Shamu. 22 Tazama, atapanda na kuruka kama tai, na kutandaza mabawa yake juu ya Bozra; na mioyo ya mashujaa wa Edomu siku hiyo itakuwa kama moyo wa mwanamke katika utungu wake. 23 Habari za Dameski. Hamathi umetahayarika, na Arpadi pia; Maana wamesikia habari mbaya; Wameyeyuka kabisa; Huzuni iko baharini, haiwezi kutulia. 24 Dameski umedhoofika; Umejigeuza kukimbia; tetemko limeushika; Dhiki na huzuni zimeupata, Kama za mwanamke katika utungu wake. 25 Imekuwaje mji wa sifa haukuachwa, mji wa furaha yangu? 26 Kwa hiyo vijana wake wataanguka katika njia kuu zake, na watu wote wa vita watanyamazishwa katika siku hiyo, asema Bwana wa majeshi. 27 Nami nitawasha moto katika ukuta wa Dameski, nao utayateketeza majumba ya Ben-hadadi. 28 Habari za Kedari, na za falme za Hazori, ambazo Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alizipiga. Bwana asema hivi, Ondokeni, pandeni hata Kedari, mkawateke nyara wana wa mashariki. 29 Hema zao na makundi yao watayatwaa; watachukulia mbali mapazia yao kwa faida yao wenyewe, na vyombo vyao vyote, na ngamia zao; nao watawapigia kelele wakisema, Hofu ziko pande zote. 30 Kimbieni ninyi, enendeni mbali mkitanga-tanga, kaeni chini sana, enyi mkaao Hazori, asema Bwana; maana Nebukadreza, mfalme wa Babeli, amefanya shauri juu yenu, naye amekusudia neno juu yenu. 31 Ondokeni, pandeni hata taifa lililo katika hali ya raha, likaalo bila kuhangaika, asema Bwana; wasio na malango wala makomeo, wakaao peke yao. 32 Na ngamia zao watakuwa mateka, na wingi wa makundi yao utakuwa nyara; nami nitawatawanya hata pepo zote watu wale wanyoao denge; nami nitaleta msiba wao toka pande zao zote, asema Bwana. 33 Na Hazori utakuwa kao la mbwa-mwitu; ukiwa milele; hapana mtu atakayekaa huko, wala hapana mwanadamu atakayekaa huko kama mgeni akaavyo. 34 Neno la Bwana lililomjia Yeremia, nabii, juu ya Elamu, mwanzo wa kumiliki kwake Sedekia, mfalme wa Yuda, kusema, 35 Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama nitauvunja upinde wa Elamu, ulio mkuu katika nguvu zao. 36 Na juu ya Elamu nitazileta pepo nne, toka pembe nne za mbinguni, nami nitawatawanya hata pepo nne zote, wala hapana taifa ambalo hawatalifikilia watu wa Elamu waliofukuzwa. 37 Nami nitawafadhaisha watu wa Elamu mbele ya adui zao, na mbele ya hao wanaowatafuta roho zao; nami nitawaletea mabaya, naam, hasira yangu kali, asema Bwana; nami nitautuma upanga uwafuatie, hata nitakapowaangamiza; 38 nami nitaweka kiti changu cha enzi huko Elamu, nami nitawaharibu, mfalme na wakuu, watoke huko, asema Bwana. 39 Lakini itakuwa, katika siku za mwisho, nitawarudisha wafungwa wa Elamu, asema Bwana.

Yeremia 50

1 Neno hili ndilo alilosema Bwana, katika habari za Babeli, na katika habari za Wakaldayo, kwa kinywa cha Yeremia, nabii. 2 Tangazeni katika mataifa, Mkahubiri na kutweka bendera; Hubirini, msifiche, semeni, Babeli umetwaliwa! Beli amefedheheka; Merodaki amefadhaika; Sanamu zake zimeaibishwa, Vinyago vyake vimefadhaika. 3 Maana toka kaskazini taifa linakuja juu yake, litakaloifanya nchi yake kuwa ukiwa; wala hapana mtu atakayekaa humo; wamekimbia, wamekwenda zao, mwanadamu na mnyama pia. 4 Katika siku hizo, na wakati huo, asema Bwana, wana wa Israeli watakuja, wao na wana wa Yuda pamoja; Wataendelea njiani mwao wakilia, nao watamtafuta Bwana, Mungu wao. 5 Watauliza habari za Sayuni, na nyuso zao zitaelekea huko, wakisema, Njoni ninyi, mjiunge na Bwana, kwa agano la milele ambalo halitasahauliwa. 6 Watu wangu wamekuwa kondoo waliopotea, wachungaji wao wamewapoteza; wamewapotosha milimani; wamekwenda toka mlima hata kilima, wamesahau mahali pao pa kupumzika. 7 Watu wote waliowaona wamewala; na adui zao walisema, Sisi hatuna hatia, kwa kuwa hao wametenda dhambi juu ya Bwana, aliye kao la haki, yaani, Bwana, tumaini la baba zao. 8 Kimbieni kutoka kati ya Babeli, mkatoke katika nchi ya Wakaldayo, mkawe kama mabeberu mbele ya makundi. 9 Kwa maana juu ya Babeli nitaamsha na kuleta kusanyiko la mataifa makubwa, toka nchi ya kaskazini; nao watajipanga juu yake; kutoka huko atatwaliwa; mishale yao itakuwa kama ya mtu shujaa aliye stadi; hapana hata mmoja utakaorudi bure. 10 Nao Ukaldayo utakuwa mateka; wote wautekao watashiba, asema Bwana. 11 Kwa sababu mnafurahi, kwa sababu mnashangilia, enyi mnaouteka urithi wangu, kwa sababu mmewanda kama mtamba akanyagaye nafaka, nanyi mnalia kama farasi wenye nguvu; 12 mama yenu atatahayarika sana; yeye aliyewazaa atafadhaika; tazama, atakuwa taifa lililo nyuma katika mataifa yote, atakuwa jangwa, nchi ya ukame, na nyika. 13 Kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana haitakaliwa na mtu, bali itakuwa ukiwa mtupu; kila mtu apitaye karibu na Babeli atashangaa, atazomea kwa sababu ya mapigo yake yote. 14 Jipangeni juu ya Babeli pande zote, Ninyi nyote mpindao upinde; Mpigeni, msiuzuie hata mshale mmoja; Kwa maana amemtenda Bwana dhambi. 15 Mpigieni kelele pande zote; amejitoa; Maboma yake yameanguka, kuta zake zimebomolewa; Kwa maana ni kisasi cha Bwana; mlipizeni kisasi; Kama yeye alivyotenda, mtendeni yeye. 16 Mpanzi mkatilie mbali na Babeli, Naye ashikaye mundu wakati wa mavuno; Kwa sababu ya kuuogopa upanga uoneao, Watageuka kila mtu kwa watu wake, Nao wataikimbilia kila mmoja nchi yake. 17 Israeli ni kondoo aliyetawanywa; simba wamemfukuzia mbali; kwanza mfalme wa Ashuru amemla, na mwisho Nebukadreza huyu, mfalme wa Babeli, amemvunja mifupa yake. 18 Basi, Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Tazama, mimi nitamwadhibu mfalme wa Babeli, na nchi yake, kama nilivyomwadhibu mfalme wa Ashuru. 19 Nami nitamleta Israeli tena malishoni kwake, naye atalisha juu ya Karmeli, na Bashani, na nafsi yake itashiba juu ya milima ya Efraimu, na katika Gileadi. 20 Katika siku hizo na wakati huo, asema Bwana, uovu wa Israeli utatafutwa, wala uovu hapana; na dhambi za Yuda zitatafutwa, wala hazitaonekana; maana nitawasamehe wale niwaachao kuwa mabaki. 21 Panda juu ya nchi ya Merathaimu, naam, juu yake, na juu yao wakaao Pekodi; ua, ukaangamize nyuma yao, asema Bwana, ukatende kama nilivyokuagiza, yote pia. 22 Pana mshindo wa vita katika nchi, Mshindo wa uharibifu mkuu. 23 Imekuwaje nyundo ya dunia yote Kukatiliwa mbali na kuvunjwa? Imekuwaje Babeli kuwa ukiwa Katikati ya mataifa? 24 Nimekutegea mtego, Ee Babeli, nawe ukanaswa, nawe ulikuwa huna habari; umeonekana, ukakamatwa, kwa sababu ulishindana na Bwana. 25 Bwana amefungua akiba yake ya silaha, naye amezitoa silaha za ghadhabu yake; maana Bwana, Bwana wa majeshi, ana kazi atakayofanya katika nchi ya Wakaldayo. 26 Njoni juu yake toka mpaka ulio mbali; Zifungueni ghala zake; Mfanyeni kuwa magofu na kumharibu kabisa; Msimsazie kitu cho chote. 27 Wachinjeni mafahali wake wote; Na watelemkie machinjoni; Ole wao! Maana siku yao imewadia, Wakati wa kujiliwa kwao. 28 Sauti yao wakimbiao na kuokoka, Kutoka katika nchi ya Babeli, Ili kutangaza Sayuni kisasi cha Bwana, Mungu wetu, Kisasi cha hekalu lake. 29 Waiteni wapiga mishale juu ya Babeli, Naam, wote waupindao upinde; Pangeni hema kumzunguka pande zote; Ili asiokoke hata mtu mmoja wao; Mlipeni kwa kadiri ya kazi yake; Mtendeni sawasawa na yote aliyoyatenda; Kwa sababu amefanya kiburi juu ya Bwana, Juu yake aliye Mtakatifu wa Israeli. 30 Kwa sababu hiyo vijana wake wataanguka katika njia kuu zake, na watu wake wa vita, wote pia, watanyamazishwa katika siku hiyo, asema Bwana. 31 Tazama, mimi ni juu yako, Ewe mwenye kiburi, asema Bwana, Bwana wa majeshi; maana siku yako imewadia, wakati nitakapokujilia. 32 Na mwenye kiburi atajikwaa, na kuanguka, wala hapana atakayemwinua; nami nitawasha moto katika miji yake, nao utawala wote wamzungukao pande zote. 33 Bwana wa majeshi asema hivi, Wana wa Israeli, na wana wa Yuda, wameonewa pamoja; na wote waliowachukua mateka wanawashika sana; wanakataa kuwaacha. 34 Mkombozi wao ni hodari; Bwana wa majeshi ndilo jina lake; yeye atawatetea kwa bidii, apate kuistarehesha nchi, na kuwasumbua wakaao katika Babeli. 35 Upanga u juu ya Wakaldayo, asema Bwana, na juu yao wakaao Babeli, na juu ya wakuu wake, na juu ya watu wake wenye hekima. 36 Upanga u juu ya hao wajisifuo, nao watapumbazika; upanga u juu ya mashujaa wake, nao watafadhaika. 37 Upanga u juu ya farasi zao, na juu ya magari yao ya vita; na juu ya watu wote waliochanganyika ndani yake, nao watakuwa kama wanawake; upanga u juu ya hazina zake, nazo zitaibwa. 38 Ukosefu wa mvua u juu ya maji yake, nayo yatakaushwa; maana ni nchi ya sanamu za kuchongwa, nao wameingiwa na wazimu kwa ajili ya sanamu. 39 Basi, wanyama wakali wa jangwani, pamoja na mbwa-mwitu, watakaa huko, na mbuni watakaa ndani yake; wala haitakaliwa na watu milele; wala hapana mtu atakayekaa huko tangu kizazi hata kizazi. 40 Kama vile vilivyotokea Mungu alipoangusha Sodoma na Gomora, na miji iliyokuwa karibu nayo, asema Bwana; kadhalika hapana mtu atakayekaa huko, wala hapana mwanadamu atakayekaa huko kama wageni wakaavyo. 41 Angalia, watu wanakuja watokao kaskazini; na taifa kubwa, na wafalme wengi wataamshwa toka pande za mwisho za dunia. 42 Wanashika upinde na mkuki; Ni wakatili, hawana huruma; Sauti yao inanguruma kama bahari, Nao wamepanda farasi; Kila mmoja amejipanga kama aendaye vitani, Juu yako, Ee binti Babeli. 43 Mfalme wa Babeli amesikia habari zao, Na mikono yake imekuwa dhaifu; Dhiki imemshika, na maumivu, Kama ya mwanamke katika utungu wake. 44 Angalia, atapanda kama simba toka kiburi cha Yordani juu ya malisho yasiyonyauka; lakini nitamkimbiza ghafula ayaache; na yeye aliye mteule nitamweka juu yake; maana ni nani aliye kama mimi? Tena ni nani atakayeniandikia muda? Tena ni mchungaji yupi atakayesimama mbele zangu? 45 Basi, lisikieni shauri la Bwana, Alilolifanya juu ya Babeli; Na makusudi yake aliyoyakusudia Juu ya nchi ya Wakaldayo. Hakika watawaburura, naam, wadogo wa kundi; Hakika malisho yao yatafadhaika kwa ajili yao. 46 Kwa mshindo wa kutwaliwa Babeli nchi yatetemeka, Na kilio chake chasikiwa katika mataifa.

Yeremia 51

1 Bwana asema hivi, Angalia, nitaamsha juu ya Babeli, na juu yao wakaao Leb-kamai upepo uharibuo. 2 Nami nitapeleka wageni mpaka Babeli, watakaompepea; nao wataifanya nchi yake kuwa tupu; kwa kuwa katika siku ya taabu watakuwa juu yake pande zote. 3 Juu yake apindaye upinde, mwenye upinde na apinde upinde wake, na juu yake ajiinuaye katika dirii yake; msiwaachilie vijana wake; liangamizeni jeshi lake lote. 4 Nao wataanguka, hali ya kuuawa, katika nchi ya Wakaldayo, hali ya kutumbuliwa katika njia kuu zake. 5 Kwa maana Israeli, wala Yuda, hakuachwa na Mungu wake, Bwana wa majeshi; ijapokuwa nchi yao imejaa hatia juu yake aliye Mtakatifu wa Israeli. 6 Kimbieni kutoka kati ya Babeli, kila mtu na ajiokoe nafsi yake; msikatiliwe mbali katika uovu wake; maana ni wakati wa kisasi cha Bwana, atamlipa malipo. 7 Babeli umekuwa kikombe cha dhahabu mkononi mwa Bwana; kilicholevya dunia yote; mataifa wamekunywa mvinyo wake; kwa sababu hiyo mataifa wameingiwa na wazimu. 8 Babeli umeanguka na kuangamia ghafula; mpigieni yowe; twaeni zeri kwa maumivu yake; ili labda apate kuponywa. 9 Tungependa kuuponya Babeli, Lakini haukuponyeka; Mwacheni, nasi twendeni zetu, Kila mtu hata nchi yake mwenyewe; Maana hukumu yake inafika hata mbinguni, Nayo imeinuliwa kufikilia mawinguni. 10 Bwana ameitokeza haki yetu; Njoni, tutangaze katika Sayuni Habari za kazi ya Bwana, Mungu wetu. 11 Inoeni hiyo mishale; zishikeni ngao kwa nguvu; Bwana ameziamsha roho za wafalme wa Wamedi; kwa sababu shauri lake ni juu ya Babeli auangamize; maana ni kisasi cha Bwana, kisasi cha hekalu lake. 12 Twekeni bendera juu ya kuta za Babeli, yatieni malindo nguvu, wawekeni walinzi, tengenezeni waviziao; kwa maana Bwana ameazimia na kutenda yote aliyoyasema juu yao wakaao Babeli. 13 Ewe ukaaye juu ya maji mengi, uliye na hazina nyingi, mwisho wako umewadia, kadiri ya tamaa zako. 14 Bwana wa majeshi ameapa kwa nafsi yake, akisema, Hakika nitakujaza watu, kama nzige, nao watapiga kelele juu yako. 15 Ameiumba dunia kwa uweza wake, Ameuthibitisha ulimwengu kwa hekima yake, Na kwa ufahamu wake amezitandika mbingu. 16 Atoapo sauti yake pana mshindo wa maji mbinguni, Naye hupandisha mawingu toka ncha za nchi; Huifanyia mvua umeme, Huutoa upepo katika hazina zake. 17 Kila mtu amekuwa kama mnyama, hana maarifa; Kila mfua dhahabu amefedheheshwa na sanamu yake ya kuchonga; Maana sanamu yake ya kuyeyuka ni uongo, Wala hamna pumzi ndani yake. 18 Ni ubatili tu, ni kazi za udanganyifu; Wakati wa kujiliwa kwao watapotea. 19 Yeye, Fungu la Yakobo, siye kama hawa; Maana ndiye aliyeviumba vitu vyote; Na Israeli ni kabila ya urithi wake; Bwana wa majeshi ndilo jina lake. 20 Wewe u rungu langu na silaha zangu za vita; kwa wewe nitawavunja-vunja mataifa; na kwa wewe nitaharibu falme; 21 na kwa wewe nitamvunja-vunja farasi, na yeye ampandaye; na kwa wewe nitalivunja-vunja gari la vita, na yeye achukuliwaye ndani yake; 22 na kwa wewe nitawavunja-vunja mwanamume na mwanamke; na kwa wewe nitawavunja-vunja mzee na mtoto; na kwa wewe nitawavunja-vunja kijana mwanamume na kijana mwanamke; 23 na kwa wewe nitamvunja-vunja mchungaji na kundi lake; na kwa wewe nitamvunja-vunja mkulima na jozi yake ya ng'ombe; na kwa wewe nitawavunja-vunja maliwali na maakida. 24 Nami nitamlipa Babeli, na wote wakaao ndani ya Ukaldayo, mabaya yao yote, waliyoyatenda katika Sayuni mbele ya macho yenu, asema Bwana. 25 Tazama, mimi ni juu yako, Ee mlima uharibuo, asema Bwana; wewe uiharibuye dunia nzima; nami nitaunyosha mkono wangu juu yako, na kukufingirisha chini toka majabalini; nami nitakufanya kuwa mlima ulioteketezwa. 26 Wala hawatatwaa kwako jiwe moja liwe la pembeni, wala jiwe moja liwe msingi; bali wewe utakuwa ukiwa daima, asema Bwana. 27 Itwekeni bendera katika nchi, pigeni tarumbeta kati ya mataifa, yawekeni mataifa tayari juu yake; ziiteni juu yake falme za Ararati, na Mini, na Ashkenazi; agizeni jemadari juu yake; wapandisheni farasi, kama tunutu. 28 Wekeni mataifa tayari juu yake, wafalme wa Wamedi, na maliwali wake, na maakida wake, na nchi yote ya mamlaka yake. 29 Nayo nchi yatetemeka, nayo ina utungu; maana makusudi ya Bwana juu ya Babeli yasimama, kuifanya nchi ya Babeli ukiwa, isikaliwe na mtu. 30 Mashujaa wa Babeli wameacha kupigana; Wanakaa katika ngome zao; Ushujaa wao umewapungukia; Wamekuwa kama wanawake; Makao yake yameteketea; Makomeo yake yamevunjika. 31 Tarishi mmoja atapiga mbio kumlaki mwingine, Na mjumbe mmoja atapiga mbio kumlaki mwenziwe, Ili kumpasha habari mfalme wa Babeli, Ya kuwa mji wake umetwaliwa kila upande. 32 Navyo vivuko vimeshambuliwa, Nayo makangaga wameyatia moto, Nao watu wa vita wameingiwa na hofu. 33 Kwa maana Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi; Binti Babeli amekuwa kama sakafu ya kufikichia wakati wa kukanyagwa kwake; bado kitambo kidogo na wakati wa mavuno utafika kwake. 34 Nebukadreza, mfalme wa Babeli, amenila, ameniseta, amenifanya kuwa chombo kitupu; amenimeza kama joka, amelijaza tumbo lake vitu vyangu vya anasa; amenitupa 35 Udhalimu niliotendwa mimi, na uliotendwa mwili wangu, umpate Babeli; ndivyo atakavyosema yeye akaaye Sayuni; na Yerusalemu atasema, Damu yangu na iwe juu yao wakaao katika Ukaldayo. 36 Basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitakutetea, nami nitatwaa kisasi kwa ajili yako; nami nitaikausha bahari yake, nitaifanya chemchemi yake kuwa pakavu. 37 Na Babeli utakuwa magofu, makao ya mbwa-mwitu, ajabu, na mazomeo, pasipo mtu wa kukaa huko. 38 Watanguruma pamoja kama wana-simba; watanguruma kama simba wachanga. 39 Wakiingiwa na ukali, nitawafanyizia karamu yao, nami nitawalevya, wapate kufurahi, na kulala usingizi wa milele, wasiamke tena, asema Bwana. 40 Nitawatelemsha kama wana-kondoo machinjoni, kama kondoo waume pamoja na mabeberu. 41 Jinsi Sheshaki alivyotwaliwa! Naye sifa ya dunia yote alivyoshambuliwa! Jinsi Babeli alivyokuwa ukiwa katikati ya mataifa. 42 Bahari imefika juu ya Babeli, Umefunikwa kwa wingi wa mawimbi yake. 43 Miji yake imekuwa maganjo; Nchi ya ukame, na jangwa; Nchi asimokaa mtu ye yote, Wala hapiti mwanadamu huko. 44 Nami nitafanya hukumu juu ya Beli katika Babeli, nami nitavitoa katika kinywa chake alivyovimeza; wala mataifa hawatamwendea tena; naam, ukuta wa Babeli utaanguka. 45 Enyi watu wangu; tokeni katikati yake, mkajiokoe nafsi zenu na hasira kali ya Bwana, kila mmoja wenu. 46 Wala isizimie mioyo yenu, wala msiiogope habari itakayosikiwa katika nchi; maana habari itakuja mwaka mmoja, na baadaye mwaka wa pili habari itakuja, na udhalimu katika nchi, mwenye kutawala akishindana na mwenye kutawala. 47 Basi angalia, siku zitakuja, ambazo katika siku hizo, nitafanya hukumu juu ya sanamu za Babeli, na nchi yake yote itatahayarika; na watu wake wote waliouawa wataanguka katikati yake. 48 Ndipo mbingu, na nchi, na vitu vyote vilivyomo, vitaimba kwa furaha juu ya Babeli; kwa maana watu waangamizao watamjilia kutoka kaskazini, asema Bwana. 49 Kama vile Babeli alivyowaangusha watu wa Israeli waliouawa, ndivyo watakavyoanguka katika Babeli watu wa nchi yake nzima waliouawa. 50 Ninyi mliojiepusha na upanga, Enendeni zenu, msisimame; Mkumbukeni Bwana tokea mbali, Na Yerusalemu ukatiwe mioyoni mwenu. 51 Twaona haya kwa kuwa tumesikia mashutumu; Fedheha imetufunikiza nyuso zetu; Kwa sababu wageni wamepaingia Patakatifu pa nyumba ya Bwana. 52 Kwa sababu hiyo siku zinakuja, asema Bwana, nitakapozihukumu sanamu zake; na katika nchi yake yote waliojeruhiwa wataugua. 53 Babeli ujapopanda mbinguni, na ujapopafanya mahali pa juu penye nguvu zake kuwa ngome, hata hivyo toka kwangu wenye kuangamiza watamwendea, asema Bwana. 54 Sauti ya kilio kutoka Babeli, Na ya uangamivu mkuu toka nchi ya Wakaldayo! 55 Maana Bwana amwangamiza Babeli, Na kuikomesha sauti kuu ndani yake; Na mawimbi yake yavuma kama maji mengi, Mshindo wa sauti zao wafanya makelele; 56 Kwa maana mwenye kuangamiza amefika kwake; Naam, amefika Babeli; Na mashujaa wake wametwaliwa; Pinde zao zimevunjika kabisa; Maana Bwana ni Mungu wa kisasi; Hakika yake yeye atalipa. 57 Nami nitawalevya wakuu wake, na watu wake wenye hekima, maliwali wake, na maakida wake, na mashujaa wake; nao watalala usingizi wa milele, wasiamke, asema Mfalme, Bwana wa majeshi, ambaye jina lake ni Bwana. 58 Bwana wa majeshi asema hivi, Kuta pana za Babeli zitabomolewa kabisa, na malango yake marefu yatateketezwa; nao watu watajitaabisha kwa ubatili, na mataifa kwa moto; nao watachoka. 59 Neno ambalo Yeremia, nabii, alimwamuru Seraya, mwana wa Neria, mwana wa Maaseya, alipokwenda Babeli pamoja na Sedekia, mfalme wa Yuda, katika mwaka wa nne wa kumiliki kwake. Basi Seraya alikuwa msimamizi mkuu wa nyumba ya mfalme. 60 Naye Yeremia akaandika katika kitabu habari ya mabaya yote yatakayoupata Babeli, maneno hayo yote yaliyoandikwa juu ya Babeli. 61 Naye Yeremia akamwambia Seraya, Utakapofika Babeli, basi angalia uyasome maneno haya yote, 62 ukaseme, Ee Bwana, umenena habari za mji huu kwamba utakatiliwa mbali, usikaliwe na awaye yote, wala wanadamu wala wanyama, lakini uwe ukiwa hata milele. 63 Tena itakuwa utakapokwisha kukisoma kitabu hicho, utakifungia jiwe, na kukitupa katika mto Frati; 64 nawe utasema, Hivyo ndivyo utakavyozama Babeli, wala hautazuka tena, kwa sababu ya mabaya yote nitakayoleta juu yake; nao watachoka. Maneno ya Yeremia yamefika hata hapa.

Yeremia 52

1 Sedekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja hapo alipoanza kumiliki; naye akamiliki miaka kumi na mmoja huko Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Hamutali, binti Yeremia wa Libna. 2 Naye alitenda yaliyo mabaya machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyatenda Yehoyakimu. 3 Maana, kwa sababu ya hasira ya Bwana, mambo haya yalitokea katika Yerusalemu na katika Yuda, hata akawaondosha wasiwe mbele za uso wake, naye Sedekia akamwasi mfalme wa Babeli. 4 Ikawa, katika mwaka wa kenda wa kumiliki kwake, katika mwezi wa kumi, na siku ya kumi ya mwezi huo, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akaja, yeye na jeshi lake lote, juu ya Yerusalemu, akapanga hema zake juu yake; nao wakajenga ngome juu yake pande zote. 5 Basi mji huo ulihusuriwa hata mwaka wa kumi na mmoja wa mfalme Sedekia. 6 Katika mwezi wa nne, siku ya kenda ya mwezi, njaa ilizidi sana ndani ya mji, hata hapakuwa na chakula kwa watu wa nchi. 7 Ukuta wa mji ukabomolewa, watu wote wa vita wakakimbia, wakatoka mjini usiku, kwa njia ya lango lililokuwa kati ya zile kuta mbili, karibu na bustani ya mfalme; (basi wale Wakaldayo walikuwa wameuzunguka mji pande zote;) wakaenda zao kwa njia ya Araba. 8 Lakini jeshi la Wakaldayo wakamfuatia mfalme, wakampata Sedekia katika nchi tambarare ya Yeriko, na jeshi lake lote walikuwa wametawanyika na kumwacha. 9 Nao wakamshika mfalme, wakamchukua kwa mfalme wa Babeli, aliyekuwa huko Ribla katika nchi ya Hamathi, naye akatoa hukumu juu yake. 10 Ndipo mfalme wa Babeli akawaua wana wa Sedekia mbele ya macho yake; pia akawaua wakuu wote wa Yuda huko Ribla. 11 Akampofusha macho Sedekia; tena mfalme wa Babeli akamfunga kwa pingu, akamchukua mpaka Babeli, akamtia gerezani hata siku ya kufa kwake. 12 Basi katika mwezi wa tano, siku ya kumi ya mwezi, ndio mwaka wa kumi na kenda wa mfalme Nebukadreza, mfalme wa Babeli; Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, aliyesimama mbele ya mfalme wa Babeli, aliingia Yerusalemu. 13 Akaiteketeza nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme; na nyumba zote za Yerusalemu, naam, kila nyumba kubwa aliiteketeza kwa moto. 14 Na jeshi lote la Wakaldayo, waliokuwa pamoja na huyo amiri wa askari walinzi, wakazibomoa kuta zote za Yerusalemu pande zote. 15 Kisha Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawachukua wafungwa baadhi ya watu waliokuwa maskini, na mabaki ya watu walioachwa katika mji, nao wale walioasi na kumkimbilia mfalme wa Babeli, nao mabaki ya vibarua. 16 Lakini Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawaacha watu walio maskini kabisa ili wawe watunza mizabibu na wakulima. 17 Na nguzo za shaba zilizokuwa katika nyumba ya Bwana, na matako ya bahari ya shaba iliyokuwa katika nyumba ya Bwana, Wakaldayo walivivunja vipande vipande, wakaichukua shaba yake yote mpaka Babeli. 18 Nayo masufuria, na majembe, na makasi, na mabakuli, na miiko, na vyombo vyote vya shaba walivyokuwa wakivitumia, wakavichukua vyote. 19 Navyo vikombe, na vyombo vya kutolea majivu, na mabakuli, na masufuria, na vinara, na miiko, na vyetezo, vilivyokuwa vya dhahabu katika dhahabu, na vilivyokuwa vya fedha katika fedha, amiri wa askari walinzi akavichukua. 20 Nguzo mbili, bahari moja, na ng'ombe kumi na mbili za shaba zilizokuwa chini ya matako yake, ambavyo mfalme Sulemani aliifanyia nyumba ya Bwana; shaba ya vitu hivyo vyote ilikuwa haiwezi kupimwa kwa kuwa nyingi sana. 21 Na nguzo hizo, urefu wa nguzo moja ulikuwa dhiraa kumi na nane, na uzi wa dhiraa kumi na mbili ungeweza kuizunguka; na unene wake ulikuwa nyanda nne; nayo ilikuwa ya uvungu. 22 Nayo ilikuwa na kichwa cha shaba juu yake; na urefu wa kichwa kimoja ulikuwa dhiraa tano; palikuwa na mapambo ya wavu na makomamanga juu ya kichwa hicho pande zote; vyote vilikuwa vya shaba; nayo nguzo ya pili ilikuwa na mapambo kama hayo, na makomamanga. 23 Palikuwa na makomamanga tisini na sita katika pande zake; makomamanga; yote yalikuwa mia juu ya wavu huo pande zote. 24 Naye amiri wa askari walinzi akamtwaa Seraya, kuhani mkuu, na Sefania, kuhani wa pili, na wale walinzi watatu wa mlango; 25 na katika mji akatwaa towashi mmoja aliyewasimamia watu wa vita; na watu saba katika wale waliouona uso wa mfalme, walioonekana katika mji; na karani wa jemadari wa jeshi, aliyewaandika watu wa nchi; na watu sitini katika watu wa nchi, walioonekana ndani ya mji. 26 Na Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawatwaa, akawaleta kwa mfalme wa Babeli huko Ribla. 27 Naye mfalme wa Babeli akawapiga na kuwaua huko Ribla katika nchi ya Hamathi. Ndivyo Yuda alivyochukuliwa utumwani, akatolewa katika nchi yake. 28 Watu hawa ndio wale ambao Nebukadreza aliwachukua mateka; katika mwaka wa saba, Wayahudi elfu tatu na ishirini na watatu; 29 katika mwaka wa kumi na nane wa Nebukadreza aliwachukua toka Yerusalemu watu mia nane na thelathini na wawili; 30 katika mwaka wa ishirini na tatu wa Nebukadreza, Nebuzaradani, amiri wa askari walinzi, akawachukua mateka katika Wayahudi watu mia saba na arobaini na watano; jumla ya watu hao wote ni watu elfu nne na mia sita. 31 Hata ikawa, katika mwaka wa thelathini na saba wa kuhamishwa kwake Yehoyakini, mfalme wa Yuda, katika mwezi wa kumi na mbili, siku ya ishirini na tano ya mwezi, Evil-merodaki, mfalme wa Babeli, katika mwaka wa kwanza wa kumiliki kwake, akamwinua kichwa chake Yehoyakini, mfalme wa Yuda, akamtoa gerezani. 32 Akasema naye maneno mazuri, akaweka kiti chake juu ya viti vya wafalme waliokuwa pamoja naye huko Babeli. 33 Naye akabadili mavazi yake ya gerezani, akala chakula mbele yake daima, siku zote za maisha yake. 34 Na kwa posho yake, alipewa posho ya daima na mfalme wa Babeli; kila siku alipewa posho hata siku ya kufa kwake, siku zote za maisha yake.

Maombolezo 1

1 Jinsi mji huu ukaavyo ukiwa, Huo uliokuwa umejaa watu! Jinsi alivyokuwa kama mjane, Yeye aliyekuwa mkuu kati ya mataifa! Binti mfalme kati ya majimbo, Jinsi alivyoshikwa shokoa! 2 Hulia sana wakati wa usiku, Na machozi yake yapo mashavuni; Miongoni mwa wote waliompenda Hakuna hata mmoja amfarijiye; Rafiki zake wote wamemtenda hila, Wamekuwa adui zake. 3 Yuda amehamishwa kwa sababu ya kuonewa, Na kwa sababu ya utumwa mkuu; Anakaa kati ya makafiri, Haoni raha iwayo yote; Wote waliomfuata wamempata Katika dhiki yake. 4 Njia za Sayuni zaomboleza, Kwa kuwa hakuna ajaye kwa sikukuu; Malango yake yote yamekuwa ukiwa, Makuhani wake hupiga kite; Wanawali wake wanahuzunika; Na yeye mwenyewe huona uchungu. 5 Watesi wake wamekuwa kichwa, Adui zake hufanikiwa; Kwa kuwa Bwana amemtesa Kwa sababu ya wingi wa makosa yake; Watoto wake wadogo wamechukuliwa mateka Mbele yake huyo mtesi. 6 Naye huyo binti Sayuni Enzi yake yote imemwacha; Wakuu wake wamekuwa kama ayala Wasioona malisho; Nao wamekwenda zao hawana nguvu Mbele yake anayewafuatia. 7 Siku za mateso na misiba yake, Yerusalemu huyakumbuka matamaniko yake yote Yaliyokuwa tangu siku za kale; Hapo watu wake walipoanguka mikononi mwa mtesi, Wala hakuna hata mmoja wa kumsaidia; Hao watesi wake walimwona, Wakafanya sabato zake kuwa mzaha. 8 Yerusalemu amefanya dhambi sana; Kwa hiyo amekuwa kama kitu kichafu; Wote waliomheshimu wanamdharau, Kwa sababu wameuona uchi wake; Naam, yeye anaugua, Na kujigeuza aende nyuma. 9 Uchafu wake ulikuwa katika marinda yake; Hakukumbuka mwisho wake; Kwa hiyo ameshuka kwa ajabu; Yeye hana mtu wa kumfariji; Tazama, Bwana, teso langu; Maana huyo adui amejitukuza. 10 Huyo mtesi amenyosha mkono wake Juu ya matamaniko yake yote; Maana ameona ya kuwa makafiri wameingia Ndani ya patakatifu pake; Ambao kwa habari zao wewe uliamuru Wasiingie katika kusanyiko lako. 11 Watu wake wote hupiga kite, Wanatafuta chakula; Wameyatoa matamaniko yao wapate chakula Cha kuihuisha nafsi; Ee Bwana, tazama, uangalie; Kwa maana mimi nimekuwa mnyonge. 12 Je! Si kitu kwenu, enyi nyote mpitao njia, Angalieni, mtazame Kama kuna majonzi yo yote mfano wa majonzi yangu, Niliyotendwa mimi, Ambayo Bwana amenihuzunisha kwa hayo Siku ya hasira yake iwakayo. 13 Toka juu amepeleka moto mifupani mwangu, Nao umeishinda; Ametandika wavu aninase miguu, Amenirudisha nyuma; Amenifanya kuwa mtu wa pekee, Na mgonjwa mchana kutwa. 14 Kongwa la makosa yangu limefungwa na mkono wake; Hayo yameshikamana; Yamepanda juu shingoni mwangu; Amezikomesha nguvu zangu; 15 Bwana amenitia mikononi mwao, Ambao siwezi kupingamana nao. Bwana amewafanya mashujaa wangu wote Kuwa si kitu kati yangu; Ameita mkutano mkuu kinyume changu Ili kuwaponda vijana wangu; Bwana amemkanyaga kama shinikizoni Huyo bikira binti Yuda. 16 Mimi ninayalilia mambo hayo; Jicho langu, jicho langu linachuruzika maji; Kwa kuwa mfariji yu mbali nami, Ambaye ilimpasa kunihuisha nafsi; Watoto wangu wameachwa peke yao, Kwa sababu huyo adui ameshinda. 17 Sayuni huinyosha mikono yake; Hakuna hata mmoja wa kumfariji; Bwana ametoa amri juu ya Yakobo, Kwamba wamzungukao wawe watesi wake; Yerusalemu amekuwa kati yao Kama kitu kichafu. 18 Bwana ndiye mwenye haki; Maana nimeiasi amri yake; Sikieni, nawasihi, enyi watu wote, Mkayatazame majonzi yangu; Wasichana wangu na wavulana wangu Wamechukuliwa mateka. 19 Naliwaita hao walionipenda Lakini walinidanganya; Makuhani wangu na wazee wangu Walifariki mjini; Hapo walipokuwa wakitafuta chakula ili kuzihuisha nafsi zao. 20 Angalia, Ee Bwana; maana mimi ni katika dhiki; Mtima wangu umetaabika; Moyo wangu umegeuka ndani yangu; Maana nimeasi vibaya sana; Huko nje upanga hufisha watu; Nyumbani mna kama mauti. 21 Wamesikia kwamba napiga kite; Hakuna hata mmoja wa kunifariji; Adui zangu wote wamesikia habari ya mashaka yaliyonipata; Hufurahi kwa kuwa umeyafanya hayo; Utaileta siku ile uliyoitangaza, Nao watakuwa kama mimi. 22 Huo uovu wao wote Na uje mbele zako wewe; Ukawatende wao kama ulivyonitenda mimi Kwa dhambi zangu zote; Kwa maana mauguzi yangu ni mengi sana, Na moyo wangu umezimia.

Maombolezo 2

1 Jinsi Bwana alivyomfunika binti Sayuni Kwa wingu katika hasira yake! Ameutupa toka mbinguni hata nchi Huo uzuri wa Israeli; Wala hakukikumbuka kiti cha miguu yake Katika siku ya hasira yake. 2 Bwana ameyameza makao yote ya Yakobo, Wala hakuona huruma; Ameziangusha ngome za binti Yuda Katika ghadhabu yake; Amezibomoa hata nchi Ameunajisi ufalme na wakuu wake. 3 Ameikata pembe yote ya Israeli Katika hasira yake kali; Ameurudisha nyuma mkono wake wa kuume Mbele ya hao adui, Naye amemteketeza Yakobo kama moto uwakao, Ulao pande zote. 4 Ameupinda upinde wake kama adui, Amesimama na mkono wake wa kuume kama mtesi; Naye amewaua hao wote Waliopendeza macho; Katika hema ya binti Sayuni Amemimina kani yake kama moto. 5 Bwana amekuwa mfano wa adui, Amemmeza Israeli; Ameyameza majumba yake yote, Ameziharibu ngome zake; Tena amemzidishia binti Yuda Matanga na maombolezo. 6 Naye ameondoa maskani yake kwa nguvu, Kana kwamba ni ya bustani tu; Ameziharibu sikukuu zake; Bwana amezisahauzisha katika Sayuni Sikukuu za makini na sabato; Naye amewadharau mfalme na kuhani Katika uchungu wa hasira yake. 7 Bwana ameitupilia mbali madhabahu yake, Amepachukia patakatifu pake; Amezitia katika mikono ya hao adui Kuta za majumba yake; Wamepiga kelele ndani ya nyumba ya Bwana Kama katika siku ya kusanyiko la makini. 8 Bwana amekusudia kuuharibu Ukuta wa binti Sayuni; Ameinyosha hiyo kamba, Hakuuzuia mkono wake usiangamize; Bali amefanya boma na ukuta kuomboleza; Zote pamoja hudhoofika. 9 Malango yake yamezama katika nchi; Ameyaharibu makomeo yake na kuyavunja; Mfalme wake na wakuu wake wanakaa Kati ya mataifa wasio na sheria; Naam, manabii wake hawapati maono Yatokayo kwa Bwana. 10 Wazee wa binti Sayuni huketi chini, Hunyamaza kimya; Wametupa mavumbi juu ya vichwa vyao, Wamejivika viunoni nguo za magunia; Wanawali wa Yerusalemu huinama vichwa vyao Kuielekea nchi. 11 Macho yangu yamechoka kwa machozi, Mtima wangu umetaabika; Ini langu linamiminwa juu ya nchi Kwa uharibifu wa binti ya watu wangu; Kwa sababu watoto wachanga na wanyonyao, Huzimia katika mitaa ya mji. 12 Wao huwauliza mama zao, Zi wapi nafaka na divai? Hapo wazimiapo kama waliojeruhiwa Katika mitaa ya mji, Hapo walipomiminika nafsi zao Vifuani mwa mama zao. 13 Nikushuhudie nini? Nikufananishe na nini, Ee Binti Yerusalemu? Nikusawazishe na nini, nipate kukufariji, Ee bikira binti Sayuni? Kwa maana uvunjifu wako ni mkuu kama bahari, Ni nani awezaye kukuponya? 14 Manabii wako wameona maono kwa ajili yako Ya ubatili na upumbavu Wala hawakufunua uovu wako, Wapate kurudisha kufungwa kwako; Bali wameona mabashiri ya ubatili kwa ajili yako Na sababu za kuhamishwa. 15 Hao watu wote wapitao Hukupigia makofi; Humzomea binti Yerusalemu, Na kutikisa vichwa vyao; Je! Mji huu ndio ulioitwa, Ukamilifu wa uzuri, Furaha ya dunia yote? 16 Juu yako adui zako wote Wamepanua vinywa vyao; Huzomea, husaga meno yao, Husema, Tumemmeza; Hakika siku hii ndiyo tuliyoitazamia; Tumeipata, tumeiona. 17 Bwana ameyatenda aliyoyakusudia; amelitimiza neno lake, Aliloliamuru siku za kale; Ameangusha hata chini, Wala hakuona huruma; Naye amemfurahisha adui juu yako, Ameitukuza pembe ya watesi wako. 18 Mioyo yao ilimlilia Bwana; Ee ukuta wa binti Sayuni! Machozi na yachuruzike kama mto Mchana na usiku; Usijipatie kupumzika; Mboni ya jicho lako isikome. 19 Inuka, ulalamike usiku, Mwanzo wa makesha yake; Mimina moyo wako kama maji usoni pa Bwana; Umwinulie mikono yako; Kwa uhai wa watoto wako wachanga wazimiao kwa njaa, Mwanzo wa kila njia kuu. 20 Tazama, Bwana, uangalie, Ni nani uliyemtenda hayo! Je! Wanawake wale mazao yao, Watoto waliowabeba? Je! Kuhani na nabii wauawe Katika patakatifu pa Bwana? 21 Kijana na mzee hulala chini Katika njia kuu; Wasichana wangu na wavulana wangu Wameanguka kwa upanga; Umewaua katika siku ya hasira yako; Umeua, wala hukuona huruma. 22 Umeziita kama katika siku ya mkutano wa makini; Hofu zangu zije pande zote; Wala hapana hata mmoja aliyepona wala kusalia Katika siku ya hasira ya Bwana; Hao niliowabeba na kuwalea Huyo adui yangu amewakomesha.

Maombolezo 3

1 Mimi ni mtu aliyeona mateso Kwa fimbo ya ghadhabu yake. 2 Ameniongoza na kuniendesha katika giza Wala si katika nuru. 3 Hakika juu yangu augeuza mkono wake Mara kwa mara mchana wote. 4 Amechakaza nyama yangu na ngozi yangu; Ameivunja mifupa yangu. 5 Amejenga boma juu yangu, Na kunizungusha uchungu na uchovu. 6 Amenikalisha penye giza, Kama watu waliokufa zamani. 7 Amenizinga pande zote hata siwezi kutoka; Ameufanya mnyororo wangu mzito. 8 Naam, nikilia na kuomba msaada, Huyapinga maombi yangu. 9 Ameziziba njia zangu kwa mawe yaliyochongwa; Ameyapotosha mapito yangu. 10 Alivyo kwangu ni kama dubu aoteaye, Kama simba aliye mafichoni. 11 Amezigeuza njia zangu, na kunirarua-rarua; Amenifanya ukiwa. 12 Ameupinda upinde wake, Na kunifanya niwe shabaha kwa mshale. 13 Amenichoma viuno Kwa mishale ya podo lake. 14 Nimekuwa dhihaka kwa watu wangu wote; Wimbo wao mchana kutwa. 15 Amenijaza uchungu, Amenikinaisha kwa pakanga. 16 Amenivunja meno kwa changarawe; Amenifunika majivu. 17 Umeniweka nafsi yangu mbali na amani; Nikasahau kufanikiwa. 18 Nikasema, Nguvu zangu zimepotea, Na tumaini langu kwa Bwana. 19 Kumbuka mateso yangu, na msiba wangu, Pakanga na nyongo. 20 Nafsi yangu ikali ikiyakumbuka hayo, Nayo imeinama ndani yangu. 21 Najikumbusha neno hili, Kwa hiyo nina matumaini. 22 Ni huruma za Bwana kwamba hatuangamii, Kwa kuwa rehema zake hazikomi. 23 Ni mpya kila siku asubuhi; Uaminifu wako ni mkuu. 24 Bwana ndiye fungu langu, husema nafsi yangu, Kwa hiyo nitamtumaini yeye. 25 Bwana ni mwema kwa hao wamngojeao, Kwa hiyo nafsi imtafutayo. 26 Ni vema mtu autarajie wokovu wa Bwana Na kumngojea kwa utulivu. 27 Ni vema mwanadamu aichukue nira Wakati wa ujana wake. 28 Na akae peke yake na kunyamaza kimya; Kwa sababu Bwana ameweka hayo juu yake. 29 Na atie kinywa chake mavumbini; Ikiwa yamkini liko tumaini. 30 Na amwelekezee yule ampigaye shavu lake; Ashibishwe mashutumu. 31 Kwa kuwa Bwana hatamtupa mtu Hata milele. 32 Maana ajapomhuzunisha atamrehemu, Kwa kadiri ya wingi wa huruma zake. 33 Maana moyo wake hapendi kuwatesa wanadamu. Wala kuwahuzunisha. 34 Kuwaseta chini kwa miguu Wafungwa wote wa duniani, 35 Kuipotosha hukumu ya mtu Mbele zake Aliye juu, 36 Na kumnyima mtu haki yake, Hayo Bwana hayaridhii kabisa. 37 Ni nani asemaye neno nalo likafanyika, Ikiwa Bwana hakuliagiza? 38 Je! Katika kinywa chake Aliye juu Hayatoki maovu na mema? 39 Mbona anung'unika mwanadamu aliye hai Mtu akiadhibiwa kwa dhambi zake? 40 Na tuchunguze njia zetu na kuzijaribu, Na kumrudia Bwana tena. 41 Na tumwinulie Mungu aliye mbinguni Mioyo yetu na mikono. 42 Sisi tumekosa na kuasi; Wewe hukusamehe. 43 Umetufunika kwa hasira na kutufuatia; Umeua, wala hukuona huruma. 44 Umejifunika nafsi yako kwa wingu, Maombi yetu yasipite. 45 Umetufanya kuwa takataka, na vifusi Katikati ya mataifa. 46 Juu yetu adui zetu wote Wametupanulia vinywa vyao. 47 Hofu imetujilia na shimo, Ukiwa na uharibifu. 48 Jicho langu lachuruzika mito ya maji Kwa ajili ya uvunjifu wa binti ya watu wangu. 49 Jicho langu latoka machozi lisikome, Wala haliachi; 50 Hata Bwana atakapoangalia Na kutazama toka mbinguni. 51 Jicho langu lanitia huzuni nafsini mwangu, Kwa sababu ya binti zote za mji wangu. 52 Walio adui zangu bila sababu Wameniwinda sana kama ndege; 53 Wameukatilia mbali uhai wangu gerezani, Na kutupa jiwe juu yangu. 54 Maji mengi yalipita juu ya kichwa changu, Nikasema, Nimekatiliwa mbali. 55 Naliliitia jina lako, Bwana, kutoka lile shimo Liendalo chini kabisa. 56 Ukaisikia sauti yangu; usifiche sikio lako Ili usisikie pumzi yangu, kwa kilio changu. 57 Ulinikaribia siku ile nilipokulilia; Ukasema, Usiogope. 58 Ee Bwana umenitetea mateto ya nafsi yangu; Umeukomboa uhai wangu. 59 Umekuona kudhulumiwa kwangu, Ee Bwana; Unihukumie neno langu. 60 Umekiona kisasi chao chote, Na mashauri yao yote juu yangu. 61 Ee Bwana, umeyasikia matukano yao, Na mashauri yao yote juu yangu; 62 Midomo yao walioinuka juu yangu Na maazimio yao juu yangu mchana kutwa. 63 Uangalie kuketi kwao, na kuinuka kwao; Wimbo wao ndio mimi. 64 Utawalipa malipo, Ee Bwana, Sawasawa na kazi ya mikono yao. 65 Utawapa ushupavu wa moyo; Laana yako juu yao. 66 Utawafuatia kwa hasira, na kuwaangamiza Wasiwe tena chini ya mbingu za Bwana.

Maombolezo 4

1 Jinsi dhahabu ilivyoacha kung'aa, Na dhahabu iliyo safi ilivyobadilika! Mawe ya patakatifu yametupwa Mwanzo wa kila njia. 2 Wana wa Sayuni wenye thamani, Walinganao na dhahabu safi, Jinsi wanavyodhaniwa kuwa vyombo vya udongo, Kazi ya mikono ya mfinyanzi! 3 Hata mbwa-mwitu hutoa matiti, Huwanyonyesha watoto wao; Binti ya watu wangu amekuwa mkali, Mfano wa mbuni jangwani. 4 Ulimi wa mtoto anyonyaye Wagandamana na kaakaa lake kwa kiu; Watoto wachanga waomba chakula, Wala hakuna hata mmoja awamegeaye. 5 Wale waliokula vitu vya anasa Wameachwa peke yao njiani; Wale waliokuzwa kuvaa nguo nyekundu Wakumbatia jaa. 6 Maana uovu wa binti ya watu wangu ni mkubwa Kuliko dhambi ya Sodoma, Uliopinduliwa kama katika dakika moja, Wala mikono haikuwekwa juu yake. 7 Wakuu wake walikuwa safi kuliko theluji, Walikuwa weupe kuliko maziwa; Miili yao, walikuwa wekundu kuliko marijani, Na umbo lao kama yakuti samawi. 8 Nyuso zao ni nyeusi kuliko makaa; Hawajulikani katika njia kuu; Ngozi yao yagandamana na mifupa yao Imekauka, imekuwa kama mti. 9 Heri wale waliouawa kwa upanga Kuliko wao waliouawa kwa njaa; Maana hao husinyaa, wakichomwa Kwa kukosa matunda ya mashamba. 10 Mikono ya wanawake wenye huruma Imewatokosa watoto wao wenyewe; Walikuwa ndio chakula chao Katika uharibifu wa binti ya watu wangu. 11 Bwana ameitimiza kani yake, Ameimimina hasira yake kali; Naye amewasha moto katika Sayuni Ulioiteketeza misingi yake. 12 Wafalme wa dunia hawakusadiki, Wala wote wakaao duniani, Ya kwamba mtesi na adui wangeingia Katika malango ya Yerusalemu. 13 Ni kwa sababu ya dhambi za manabii wake Na maovu ya makuhani wake, Walioimwaga damu ya wenye haki Katikati yake. 14 Hutanga-tanga njiani kama vipofu, Wametiwa unajisi kwa damu; Hata ikawa watu wasiweze Kuyagusa mavazi yao. 15 Watu waliwapigia kelele, Ondokeni, Uchafu, Ondokeni, ondokeni, msiguse; Walipokimbia na kutanga-tanga, watu walisema kati ya mataifa, Hawatakaa hapa tena. 16 Hasira ya Bwana imewatenga, Yeye hatawaangalia tena; Hawakujali nafsi za wale makuhani, Hawakuwaheshimu wazee wao. 17 Macho yetu yamechoka Kwa kuutazamia bure msaada wetu; Katika kungoja kwetu tumengojea taifa Lisiloweza kutuokoa. 18 Wanatuvizia hatua zetu, Hata hatuwezi kwenda katika njia zetu; Mwisho wetu umekaribia, siku zetu zimetimia; Maana mwisho wetu umefika. 19 Waliotufuatia ni wepesi Kuliko tai za mbinguni; Hao walitufuatia milimani, Nao walituotea jangwani. 20 Pumzi ya mianzi ya pua zetu, masihi wa BWANA, Alikamatwa katika marima yao;Ambaye kwa habari zake tulisema,Chini ya kivuli chake tukakaa kati ya mataifa. 21 Furahi, ushangilie, Ee binti Edomu, Ukaaye katika nchi ya Usi; Hata kwako kikombe kitapita, Utalewa, na kujifanya uchi. 22 Uovu wako umetimia, Ee binti Sayuni; Hatakuhamisha tena; Atapatiliza uovu wako, Ee binti Edomu; Atazivumbua dhambi zako.

Maombolezo 5

1 Ee Bwana, kumbuka yaliyotupata; Utazame na kuiona aibu yetu. 2 Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni; Na nyumba zetu kuwa mali ya makafiri. 3 Tumekuwa yatima waliofiwa na baba; Mama zetu wamekuwa kama wajane. 4 Tumekunywa maji yetu kwa fedha; Kuni zetu twauziwa. 5 Watufuatiao wa juu ya shingo zetu; Tumechoka tusipate raha yo yote. 6 Tumewapa hao Wamisri mkono; Na Waashuri nao, ili tushibe chakula. 7 Baba zetu walitenda dhambi hata hawako; Na sisi tumeyachukua maovu yao. 8 Watumwa wanatutawala; Hakuna mtu wa kutuokoa na mikono yao. 9 Twapata chakula kwa kujihatarisha nafsi zetu; Kwa sababu ya upanga wa nyikani. 10 Ngozi yetu ni nyeusi kama tanuu; Kwa sababu ya hari ya njaa ituteketezayo. 11 Huwatia jeuri wanawake katika Sayuni; Na mabikira katika miji ya Yuda. 12 Wakuu hutungikwa kwa mikono yao; Nyuso za wazee hazipewi heshima. 13 Vijana huyachukua mawe ya kusagia; Na watoto hujikwaa chini ya kuni. 14 Wazee wameacha kwenda langoni; Na vijana kwenda ngomani. 15 Furaha ya mioyo yetu imekoma; Machezo yetu yamegeuka maombolezo. 16 Taji ya kichwa chetu imeanguka; Ole wetu! Kwa kuwa tumetenda dhambi. 17 Kwa sababu hiyo mioyo yetu imezimia; Kwa ajili ya hayo macho yetu hayaoni vema. 18 Kwa ajili ya mlima Sayuni ulio ukiwa, Mbweha hutembea juu yake. 19 Wewe, Bwana, unadumu milele; Kiti chako cha enzi ni tangu kizazi hata kizazi. 20 Mbona watusahau sikuzote; Na kutuacha muda huu mwingi? 21 Ee Bwana, utugeuze kwako, nasi tutageuka; Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale. 22 Isipokuwa wewe umetukataa kabisa; Nawe una hasira nyingi sana juu yetu.

Ezekieli 1

1 Ikawa katika mwaka wa thelathini, mwezi wa nne, siku ya tano ya mwezi, nilipokuwa pamoja na watu waliohamishwa, karibu na mto Kebari, mbingu zilifunuka, nikaona maono ya Mungu. 2 Siku ya tano ya mwezi, nao ulikuwa ni mwaka wa tano wa kuhamishwa kwake mfalme Yehoyakini, 3 neno la Bwana lilimjia Ezekielii, kuhani, mwana wa Buzi, kwa dhahiri, katika nchi ya Wakaldayo, karibu na mto Kebari; na mkono wa Bwana ulikuwa hapo juu yake. 4 Nikaona, na tazama, upepo wa dhoruba ulitoka upande wa kaskazini, wingu kubwa sana, pamoja na moto, ukifanya duara ya nuru, na mwangaza pande zote, na katikati yake kitu kama rangi ya kaharabu, katikati ya moto huo. 5 Kukatokea katikati yake mfano wa viumbe hai vinne. Kuonekana kwao kulikuwa hivi; walikuwa na sura ya mwanadamu. 6 Na kila mmoja alikuwa na nyuso nne, na kila mmoja alikuwa na mabawa manne. 7 Na miguu yao ilikuwa miguu iliyonyoka; na nyayo za miguu yao zilikuwa kama nyayo za miguu ya ndama; zikimetameta kama rangi ya shaba iliyosuguliwa sana. 8 Nao walikuwa na mikono ya mwanadamu chini ya mabawa yao, pande zote nne; na wote wanne walikuwa na nyuso zao na mabawa yao hivi; 9 mabawa yao yaliungana, hili na hili; nao hawakugeuka walipokwenda, walikwenda kila mmoja kuelekea mbele. 10 Kwa habari za mfano wa nyuso zao; walikuwa na uso wa mwanadamu; na hao wanne walikuwa na uso wa simba upande wa kuume; na hao wanne walikuwa na uso wa ng'ombe upande wa kushoto; na hao wanne walikuwa na uso wa tai pia. 11 Na nyuso zao na mabawa yao yalikuwa yametengana kwa juu; mabawa mawili ya kila mmoja yaliungana, hili na hili, na mawili yalifunika miili yao. 12 Nao walikwenda kuelekea mbele, kila mmoja wao; roho ilikotaka kwenda ndiko walikokwenda; hawakugeuka walipokwenda. 13 Kwa habari za kuonekana kwao vile viumbe hai; kuonekana kwao kulikuwa kama makaa ya moto yawakayo, kama kuonekana kwa vinga vya moto; moto ule ulikuwa ukienda juu na kushuka chini, katikati ya vile viumbe hai; na ule moto ulikuwa na mwangaza mwingi, na katika ule moto ulitoka umeme. 14 Na vile viumbe hai walipiga mbio, kwenda na kurudi, kama kuonekana kwa kumulika kwa umeme. 15 Basi, nilipokuwa nikivitazama vile viumbe hai, tazama, gurudumu moja juu ya nchi, karibu na kila kimoja cha vile viumbe hai, pande zake zote nne. 16 Kuonekana kwake magurudumu hayo na kazi yake kulikuwa kama rangi ya zabarajadi; nayo yote manne yalikuwa na mfano mmoja; na kuonekana kwake na kazi yake kulikuwa kana kwamba ni gurudumu ndani ya gurudumu lingine. 17 Yalipokwenda yalikwenda pande zote nne; hayakugeuka yalipokwenda. 18 Katika habari za vivimbe vyake; vilikuwa virefu, vya kutisha; nayo yote manne, vivimbe vyake vimejaa macho pande zote. 19 Na viumbe hao walipokwenda, magurudumu yalikwenda kandokando yao, na viumbe hao walipoinuliwa, magurudumu nayo yaliinuliwa. 20 Kila mahali ambako roho hiyo ilitaka kwenda, walikwenda; walikuwa na roho ya kwenda huko; nayo magurudumu yaliinuliwa karibu nao; kwa maana roho ya viumbe hai ilikuwa ndani ya magurudumu. 21 Walipokwenda hao, yalikwenda hayo nayo; na waliposimama hao, yalisimama hayo nayo; na walipoinuliwa hao juu ya nchi, magurudumu yaliinuliwa karibu nao; maana roho ya viumbe hai ilikuwa ndani ya magurudumu. 22 Tena juu ya vichwa vya viumbe hai palikuwa na kitu mfano wa anga, kama rangi ya bilauri, lenye kutisha, limetandwa juu ya vichwa vyao. 23 Na chini ya anga mabawa yao yamenyoshwa, moja kulielekea la pili; kila mmoja alikuwa na mawili yaliyowafunika miili yao upande mmoja, na kila mmoja alikuwa na mawili yaliyowafunika miili yao upande wa pili. 24 Nao walipokwenda nalisikia mshindo wa mabawa yao, kama mshindo wa maji makuu, kama sauti yake Mwenyezi, mshindo wa mvumo, kama mshindo wa jeshi; hapo waliposimama walishusha mabawa yao. 25 Tena palikuwa na sauti juu ya anga lile, lililokuwa juu ya vichwa vyao; hapo waliposimama walishusha mabawa yao. 26 Na juu ya anga, lililokuwa juu ya vichwa vyao, palikuwa na mfano wa kiti cha enzi, kuonekana kwake kama yakuti samawi; na juu ya mfano huo wa kiti cha enzi, ulikuwako mfano kama kuonekana kwa mfano wa mwanadamu juu yake. 27 Nikaona kana kwamba ni rangi ya kaharabu, kama kuonekana kwa moto ndani yake pande zote, tangu kuonekana kwa viuno vyake na juu; na tangu kuonekana kwa viuno vyake na chini, naliona kana kwamba ni kuonekana kwa moto; tena palikuwa na mwangaza pande zake zote. 28 Kama kuonekana kwa upinde wa mvua, ulio katika mawingu siku ya mvua, ndivyo kulivyokuwa kuonekana kwa mwangaza ule pande zote. Ndivyo kulivyokuwa kuonekana kwake mfano huo wa utukufu wa Bwana. Nami nilipoona nalianguka kifudifudi, nikasikia sauti ya mmoja anenaye.

Ezekieli 2

1 Akaniambia, Mwanadamu, simama kwa miguu yako, nami nitasema nawe. 2 Naye aliposema nami, roho ikaniingia, ikanisimamisha; nikamsikia yeye aliyesema nami. 3 Akaniambia, Mwanadamu, nakutuma kwa wana wa Israeli, kwa mataifa wanaoasi, walioniasi mimi; wao na baba zao wamekosa juu yangu, naam, hata hivi leo. 4 Na wana hao wana nyuso zisizo na haya, na mioyo yao ni migumu. Mimi nakutuma kwa hao; nawe utawaambia, Bwana MUNGU asema hivi. 5 Nao, kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia, (maana ndio nyumba ya kuasi hao), hata hivyo watajua ya kuwa nabii amekuwako miongoni mwao. 6 Na wewe, mwanadamu, usiwaogope hao, wala usiyaogope maneno yao, ijapokuwa miiba na michongoma i pamoja nawe, nawe unakaa katikati ya nge; usiyaogope maneno yao, wala usifadhaike kwa sababu ya nyuso zao, wajapokuwa ni nyumba yenye kuasi. 7 Nawe utawaambia maneno yangu, kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia; maana hao wanaasi sana. 8 Bali wewe, mwanadamu, sikia neno hili ninalokuambia; usiwe wewe mwenye kuasi kama nyumba ile yenye kuasi; funua kinywa chako, ule nikupacho. 9 Nami nilipotazama, mkono ulinyoshwa kunielekea; na tazama, gombo la chuo lilikuwa ndani yake. 10 Akalikunjua mbele yangu; nalo lilikuwa limeandikwa ndani na nje; ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio, na ole!

Ezekieli 3

1 Akaniambia, Mwanadamu, kula uonacho; kula gombo hili, kisha enenda ukaseme na wana wa Israeli. 2 Basi nikafunua kinywa changu, naye akanilisha lile gombo. 3 Akaniambia, Mwanadamu, lisha tumbo lako, ulijaze tumbo lako kwa hili gombo nikupalo. Ndipo nikalila, nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali. 4 Akaniambia, Mwanadamu, haya! Waendee wana wa Israeli ukawaambie maneno yangu. 5 Maana wewe hukutumwa kwa watu wa maneno mageni, ama wa lugha ngumu, bali kwa nyumba ya Israeli; 6 si kwa watu wa kabila nyingi wenye maneno mageni, na lugha ngumu, ambao huwezi kufahamu maneno yao. Bila shaka, kama ningekutuma kwa watu hao, wangekusikiliza. 7 Bali nyumba ya Israeli hawatakusikiliza wewe; kwa kuwa hawanisikilizi mimi; maana nyumba yote ya Israeli wana vipaji vigumu, na mioyo yenye ukaidi. 8 Tazama, nimeufanya uso wako kuwa mgumu juu ya nyuso zao, na kipaji cha uso chako kuwa kigumu juu ya vipaji vya nyuso vyao. 9 Kama almasi ilivyo ngumu kuliko gumegume, ndivyo nilivyokifanya kipaji chako; usiwaogope, wala usifadhaike kwa sababu ya nyuso zao, wajapokuwa ni nyumba ya kuasi. 10 Tena akaniambia, Mwanadamu, maneno yangu yote nitakayokuambia, yapokee moyoni mwako, na kuyasikia kwa masikio yako. 11 Haya! Enenda uwafikilie watu hao waliohamishwa, kwa wana wa watu wako, ukaseme nao, na kuwaambia, Bwana MUNGU asema hivi; kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia. 12 Ndipo roho ikaniinua, nami nikasikia nyuma yangu sauti kama mshindo wa radi kuu, ikisema, Na uhimidiwe utukufu wa Bwana tokea mahali pake. 13 Nikasikia mshindo wa mabawa ya vile viumbe hai, walipogusana, na mshindo wa yale magurudumu kando yao, mshindo wa radi kuu. 14 Basi roho ikaniinua, ikanichukua mahali pengine; nami nikaenda kwa uchungu, na hasira kali rohoni mwangu, na mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu kwa nguvu. 15 Ndipo nikawafikia watu waliohamishwa, huko Tel-abibu, waliokuwa wakikaa karibu na mto Kebari, nikafika huko walikokuwa wakikaa; nikaketi huko miongoni mwao muda wa siku saba, katika hali ya ushangao mwingi. 16 Hata ikawa, mwisho wa siku saba, neno la Bwana likanijia, kusema, 17 Mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi wa nyumba ya Israeli; basi, sikia neno hili litokalo katika kinywa changu, ukawape maonyo haya yatokayo kwangu. 18 Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; wewe usimpe maonyo, wala husemi na huyo mtu mbaya ili kumwonya, kusudi aache njia yake mbaya na kujiokoa roho yake; mtu yule mbaya atakufa katika uovu wake; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. 19 Lakini ukimwonya mtu mbaya, wala yeye hauachi ubaya wake, wala njia yake mbaya, atakufa katika uovu wake; bali wewe umejiokoa roho yako. 20 Tena mtu mwenye haki aiachapo haki yake, na kutenda uovu, nami nikiweka kikwazo mbele yake, atakufa; kwa sababu hukumwonya, atakufa katika uovu wake, wala matendo yake ya haki aliyoyatenda hayatakumbukwa; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. 21 Bali ukimwonya mwenye haki, kwamba yule mwenye haki asitende dhambi, tena ikiwa yeye hatendi dhambi, hakika ataishi, kwa sababu alikubali kuonywa; nawe umejiokoa roho yako. 22 Na mkono wa Bwana ulikuwako juu yangu huko; akaniambia, Ondoka, enenda uwandani; nami nitasema nawe huko. 23 Basi, nikaondoka, nikaenda uwandani, na tazama, utukufu wa Bwana ulisimama huko, kama utukufu ule niliouona karibu na mto Kebari; nami nikaanguka kifudifudi. 24 Ndipo roho ile ikaniingia, ikanisimamisha kwa miguu yangu; akasema nami, akaniambia, Enenda ukajifungie nyumbani mwako. 25 Lakini wewe, mwanadamu, tazama, watakutia pingu, nao watakufunga kwazo, wala hutakwenda nje kati yao; 26 nami nitaufanya ulimi wako ugandamane na kaakaa lako, hata utakuwa bubu, wala hutakuwa mwonyaji kwao; kwa kuwa wao ni nyumba yenye kuasi. 27 Lakini hapo nitakaposema nawe, nitafumbua kinywa chako, nawe utawaambia, Bwana MUNGU asema hivi. Yeye asikiaye na asikie; naye akataaye na akatae; maana wao ni nyumba yenye kuasi.

Ezekieli 4

1 Wewe nawe, mwanadamu, jipatie tofali uliweke mbele yako, kisha, chora juu yake mfano wa mji, yaani, Yerusalemu; 2 ukauhusuru, ukajenge ngome juu yake, na kufanya boma juu yake; ukaweke makambi juu yake, na kuweka magogo ya kuubomoa yauzunguke pande zote. 3 Kisha ukajipatie bamba la chuma, ukalisimamishe liwe ukuta wa chuma kati ya wewe na mji huo; ukaelekeze uso wako juu yake, nao utahusuriwa, nawe utauhusuru. Hili litakuwa ishara kwa nyumba ya Israeli. 4 Tena lala chini kwa ubavu wako wa kushoto, ukaweke huo uovu wa nyumba ya Israeli juu yake; kwa kadiri ya hesabu ya siku utakazolala juu yake, kwa kadiri hiyo utauchukua uovu wao. 5 Maana nimekuagizia miaka ya uovu wao iwe kwako hesabu ya siku, yaani, siku mia tatu na tisini; ndivyo utakavyouchukua uovu wa nyumba ya Israeli. 6 Tena utakapozitimiza hizo, utalala kwa ubavu wako wa kuume, nawe utauchukua uovu wa nyumba ya Yuda; siku arobaini, siku moja kwa mwaka mmoja, nimekuagizia. 7 Nawe utauelekeza uso wako, uelekee mazingiwa ya Yerusalemu, na mkono wako utakuwa haukuvikwa nguo, nawe utatoa unabii juu yake. 8 Na tazama, nitakutia pingu, wala hutageuka toka upande mmoja hata upande wa pili, hata utakapozitimiza siku za mazingiwa yako. 9 Pia ujipatie ngano, na shayiri, na kunde, na dengu, na mtama, na kusemethi, ukavitie vyote katika chombo kimoja, ukajifanyie mkate kwa vitu hivyo; kwa kadiri ya hesabu ya siku utakazolala ubavuni mwako; yaani, siku mia tatu na tisini utaula. 10 Na chakula chako utakachokula kitapimwa, shekeli ishirini kwa siku moja; utakila kwa wakati wake. 11 Nawe utakunywa maji kwa kuyapima, sehemu ya sita ya hini; utayanywa kwa wakati wake. 12 Nawe utakila kama mkate wa shayiri, nawe utakioka mbele ya macho yao juu ya mashonde yatokayo katika mwanadamu. 13 Bwana akasema, Hivyo ndivyo wana wa Israeli watakavyokula chakula chao, hali kimetiwa unajisi, kati ya mataifa nitakakowafukuza. 14 Ndipo nikasema, Ee Bwana MUNGU, tazama, roho yangu haikutiwa unajisi; maana tangu ujana wangu hata sasa sijala nyamafu, wala iliyoraruliwa na hayawani; wala nyama ichukizayo haikuingia kinywani mwangu. 15 Ndipo akaniambia, Tazama, nimekupa mashonde ya ng'ombe badala ya mashonde ya mwanadamu, nawe utakipika chakula chako juu ya hayo. 16 Tena akaniambia, Mwanadamu, tazama, nitalivunja tegemeo la chakula katika Yerusalemu; nao watakula mkate kwa kuupima, na kwa kuutunza sana; nao watakunywa maji kwa kuyapima, na kwa kushangaa; 17 wapate kupungukiwa na mkate na maji, na kustaajabiana, na kukonda kwa sababu ya uovu wao.

Ezekieli 5

1 Nawe, mwanadamu, ujipatie upanga mkali, kama wembe wa kinyozi ujipatie, ukaupitishe juu ya kichwa chako na ndevu zako; kisha ujipatie mizani ya kupimia, ukazigawanye nywele hizo. 2 Theluthi ya hizo utaiteketeza katikati ya mji, siku za mazingiwa zitakapotimia; nawe utatwaa theluthi, na kuipiga kwa upanga pande zote; nawe utatawanya theluthi ichukuliwe na upepo, nami nitafuta upanga nyuma yake. 3 Nawe twaa nywele chache katika hizo, na kuzifunga katika upindo wa mavazi yako. 4 Nawe utatwaa tena baadhi ya hizo, na kuzitupa katikati ya moto, na kuziteketeza katika moto huo; kutoka nywele hizo moto utakuja na kuingia katika nyumba yote ya Israeli. 5 Bwana MUNGU asema hivi; Huu ndio Yerusalemu; nimeuweka kati ya mataifa, na nchi zauzunguka pande zote. 6 Nao umeasi hukumu zangu, kwa kutenda mabaya kuliko mataifa hayo, nao umeasi sheria kuliko nchi hizo ziuzungukazo; maana wamezikataa hukumu zangu, wala hawakuenda katika sheria zangu. 7 Basi, kwa hiyo Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu ninyi mmefanya ghasia kuliko mataifa wawazungukao ninyi, wala hamkuenda katika sheria zangu, wala hamkuzishika hukumu zangu, wala hamkutenda kama kawaida za mataifa wawazungukao; 8 basi, Bwana MUNGU asema hivi; Angalia, mimi, naam, mimi, ni juu yako; nami nitafanya hukumu kati yako machoni pa mataifa. 9 Nami nitakutenda nisiyoyatenda zamani, wala sitafanya tena mambo kama hayo, kwa sababu ya machukizo yako yote. 10 Kwa sababu hiyo baba za watu watawala wana wao kati yako, nao wana watawala baba zao; nami nitafanya hukumu ndani yako, na hao wote waliosalia kwako nitawatawanya kwa pepo zote. 11 Kwa sababu hiyo, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hakika kwa kuwa umepatia unajisi patakatifu pangu, kwa matendo yako yote niyachukiayo, na kwa machukizo yako yote, kwa sababu hiyo mimi nami nitakupunguza; wala jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma. 12 Theluthi yenu mtakufa kwa tauni, na kwa njaa watakomeshwa ndani yako; na theluthi yenu wataanguka kwa upanga pande zako zote; na theluthi yenu nitawatawanya kwa pepo zote, kisha nitafuta upanga nyuma yao. 13 Hivyo ndivyo ghadhabu yangu itakavyotimia, nami nitatosheleza hasira yangu juu yao, nami nitafarijika; nao watajua ya kuwa mimi, Bwana, nimenena kwa wivu wangu, nitakapokuwa nimeitimiza ghadhabu yangu juu yao. 14 Tena nitakufanya kuwa ukiwa, na aibu, kati ya mataifa wakuzungukao, machoni pa watu wote wapitao. 15 Nayo itakuwa tukano na aibu, na mafundisho na ajabu, kwa mataifa wakuzungukao, hapo nitakapotekeleza hukumu ndani yako, kwa hasira, na kwa ghadhabu, na kwa malaumu ya ghadhabu; mimi, Bwana, nimeyanena hayo; 16 hapo nitakapopeleka mishale mibaya ya njaa juu yao, iletayo uharibifu, nitakayoipeleka ili kuwaharibu ninyi; nami nitaiongeza njaa juu yenu, na tegemeo lenu la mkate nitalivunja. 17 Nami nitapeleka juu yenu njaa na wanyama wabaya, nao watakunyang'anya watu wako; na tauni na damu zitapita ndani yako; nami nitauleta upanga juu yako; mimi Bwana, nimeyanena hayo.

Ezekieli 6

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, uelekeze uso wako uitazame milima ya Israeli, ukaitabirie, 3 ukisema, Enyi milima ya Israeli, lisikieni neno la Bwana MUNGU; Bwana MUNGU aiambia hivi milima na vilima, na vijito na mabonde; Tazama, mimi, naam, mimi, nitaleta upanga juu yenu, nami nitapaharibu mahali penu palipoinuka, 4 Na madhabahu zenu zitakuwa ukiwa, na sanamu zenu za jua zitavunjika; nami nitawatupa wana wenu waliouawa mbele ya vinyago vyenu. 5 Nami nitaiweka mizoga ya wana wa Israeli mbele ya vinyago vyao; nami nitaitawanya mifupa yenu pande zote za madhabahu zenu. 6 Kila mahali mkaapo miji itaharibika, na mahali palipoinuka patakuwa ukiwa; ili madhabahu zenu ziharibiwe, na kufanywa ukiwa, na vinyago vyenu vivunjwe, na kukoma, na sanamu zenu za jua zikatwe, na kuangushwa, na kazi zenu zifutwe kabisa. 7 Na hao waliouawa wataanguka katikati yenu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 8 Lakini nitasaza mabaki; maana mtakuwa na baadhi ya watu watakaoukimbia upanga kati ya mataifa, mtakapokuwa mmetawanyika katika nchi za watu. 9 Na hao wa kwenu watakaookoka watanikumbuka kati ya mataifa, watakakochukuliwa mateka, jinsi nilivyoiponda mioyo yao ya kikahaba, iliyoniacha, na macho yao, yaendayo kufanya uasherati na vinyago vyao; nao watajichukia nafsi zao machoni pao wenyewe, kwa sababu ya mabaya yao yote, waliyoyatenda kwa machukizo yao yote. 10 Nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana; sikusema bure kama nitawatenda mabaya hayo. 11 Bwana MUNGU asema hivi; Piga kwa mkono wako, ipige nchi kwa mguu wako, ukaseme, Ole! Kwa sababu ya machukizo maovu yote ya nyumba ya Israeli; maana wataanguka kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni. 12 Yeye aliye mbali sana atakufa kwa tauni; na yeye aliye karibu atakufa kwa upanga; na yeye atakayesalia, na kuhusuriwa katika mji, atakufa kwa njaa, hivyo ndivyo nitakavyoitimiza ghadhabu yangu juu yao. 13 Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, watu wa kwao waliouawa watakapokuwa kati ya vinyago vyao, pande zote za madhabahu zao, juu ya kila kilima kirefu, juu ya vilele vya milima, na chini ya kila mti wenye majani mabichi, na chini ya kila mwaloni mnene, pale pale walipovifukizia uvumba mzuri vinyago vyao vyote. 14 Nami nitanyosha mkono wangu juu yao, na kuifanya nchi kuwa maganjo, tena ukiwa mbaya kuliko jangwa upande wa Dibla, katika makao yao yote; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 7

1 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Na wewe, mwanadamu, Bwana MUNGU aiambia hivi nchi ya Israeli; Ni mwisho; mwisho umezijia pembe nne za nchi. 3 Sasa mwisho huu unakupata, nami nitakuletea hasira yangu, nitakuhukumu sawasawa na njia zako; nami nitakupatiliza machukizo yako yote. 4 Jicho langu halitakuachilia, wala sitaona huruma; bali nitakupatiliza njia zako, na machukizo yako yatakuwa katikati yako; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 5 Bwana MUNGU asema hivi; Ni jambo baya, jambo baya la namna ya peke yake; angalia, linakuja. 6 Mwisho umekuja, mwisho huu umekuja; unaamka ukupate; angalia, unakuja. 7 Ajali yako imekujia, wewe ukaaye katika nchi hii; majira yamewadia, siku ile inakaribia; siku ya fujo, wala si ya shangwe milimani. 8 Basi hivi karibu nitamwaga ghadhabu yangu juu yako, nitazitimiza hasira zangu juu yako, nami nitakuhukumu sawasawa na njia zako; nami nitakupatiliza machukizo yako yote. 9 Jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma; nitakupatiliza njia zako na machukizo yako yote yatakuwa katikati yako; nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, napiga. 10 Angalia, siku hiyo; angalia, inakuja; ajali yako imetokea; fimbo imechanua, kiburi kimechipuka. 11 Udhalimu umeinuka, ukawa fimbo ya uovu; hapana mtu atakayesalia miongoni mwao, wala katika jamii yao, wala kitu katika utajiri wao; wala hakutakuwa kutukuka kati yao. 12 Majira yamewadia, siku ile inakaribia; huyo anunuaye asifurahi, wala asihuzunike auzaye; maana ghadhabu imewapata wote jamii. 13 Kwa maana auzaye hatakirudia kilichouzwa, wajapokuwa wangali hai; kwa sababu maono haya yawahusu wote jamii; hapana mmoja atakayerudi; wala hapana mtu atakayejitia nguvu katika uovu wa maisha yake. 14 Wamepiga tarumbeta, wameweka vitu vyote tayari; lakini hapana aendaye vitani; maana ghadhabu yangu imewapata wote jamii. 15 Upanga uko nje, na tauni na njaa zimo ndani; yeye aliye nje mashambani atakufa kwa upanga; na yeye aliye ndani ya mji, njaa na tauni zitamla. 16 Lakini watakaokimbia watakimbia, nao watakuwa juu ya milima kama hua wa bondeni, wote wakilia, kila mmoja katika uovu wake. 17 Mikono yote itakuwa dhaifu, na magoti yote yatalegea kama maji. 18 Tena watajifungia nguo za magunia, na utisho utawafunika; na aibu itakuwa juu ya nyuso zote, na upaa juu ya vichwa vyao vyote. 19 Watatupa fedha yao katika njia kuu za mji, na dhahabu yao itakuwa kama kitu cha unajisi; fedha yao na dhahabu yao hazitaweza kuwaokoa siku ya ghadhabu ya Bwana; hawatajishibisha roho zao, wala hawatajijaza matumbo yao; kwa sababu zilikuwa kwazo la uovu wao. 20 Na uzuri wa pambo lake, yeye aliuweka katika enzi, lakini wao walifanya sanamu za machukizo yao, na vitu vyao vichukizavyo, ndani yake; ndiyo maana nimeifanya kuwa kama kitu cha unajisi kwao. 21 Nami nitapatia katika mikono ya wageni pawe mateka yao, na katika mikono ya waovu wa duniani pawe mawindo yao, nao watapanajisi. 22 Tena nitaugeuza uso wangu usiwaelekee, nao watapatia unajisi mahali pangu pa siri; na wanyang'anyi wataingia humo na kupatia unajisi. 23 Ufue mnyororo; kwa maana nchi hii imejaa hukumu za damu, nao mji umejaa udhalimu. 24 Kwa sababu hiyo nitawaleta watu wa mataifa walio wabaya kabisa, nao watazimiliki nyumba zao; tena nitakikomesha kiburi chao wenye nguvu; na mahali pao patakatifu patatiwa unajisi. 25 Uharibifu unakuja; nao watatafuta amani, lakini haitapatikana. 26 Madhara yatakuja juu ya madhara, na habari ya shari juu ya habari ya shari; nao watakwenda kwa nabii kutaka maono; lakini hiyo sheria itampotea kuhani, na mashauri yatawapotea wazee. 27 Mfalme ataomboleza, na mkuu atavikwa ukiwa, na mikono ya watu wa nchi itataabika; nitawatenda sawasawa na njia yao; nami nitawahukumu sawasawa na kustahili kwao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 8

1 Ikawa katika mwaka wa sita, mwezi wa sita, siku ya tano ya mwezi, nilipokuwa nikikaa nyumbani mwangu, wazee wa Yuda nao wali wamekaa mbele yangu, mkono wa Bwana MUNGU ukaniangukia huko. 2 Ndipo nikaangalia, na tazama, kana kwamba ni mfano wa moto; tangu mfano wa viuno vyake na chini, moto; na tangu mfano wa viuno vyake na juu, kana kwamba ni mfano wa mwangaza, kama rangi ya kaharabu. 3 Naye akanyosha mfano wa mkono, akanishika kwa kishungi kimoja cha nywele za kichwa changu; nayo roho ikaniinua kati ya dunia na mbingu, ikanileta katika maono ya Mungu mpaka Yerusalemu, mpaka mlango wa kuingilia ua wa ndani uelekeao upande wa kaskazini; mahali palipokuwa pamewekwa sanamu ya wivu, itiayo wivu. 4 Na tazama, huo utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwapo hapo, sawasawa na maono yale niliyoyaona katika uwanda. 5 Ndipo akaniambia, Mwanadamu, inua macho yako sasa, uangalie upande wa kaskazini. Basi nikainua macho yangu, nikaangalia upande wa kaskazini, na tazama, upande wa kaskazini wa mlango, ilikuwako sanamu ile ya wivu, mahali pale pa kuingilia. 6 Akaniambia, Mwanadamu, je! Unayaona wanayoyafanya, yaani, haya machukizo makubwa wanayoyafanya nyumba ya Israeli hapa, hata niende zangu mbali na patakatifu pangu? Lakini utaona tena machukizo makubwa mengine. 7 Akanileta hata mlango wa ua; nami nilipoangalia, tazama, pana tundu katika ukuta. 8 Ndipo akaniambia, Mwanadamu, toboa sasa katika ukuta huu; nami nilipotoboa, tazama, pana mlango. 9 Akaniambia, Ingia uyaone machukizo mabaya wanayoyafanya hapa. 10 Basi, nikaingia, nikaona; na tazama, kila namna ya wadudu, na wanyama wachukizao, na taswira za vinyago vyote vya nyumba ya Israeli, zimepigwa ukutani pande zote. 11 Na watu sabini wa wazee wa Israeli walikuwa wamesimama na kuzielekea, na katikati yao alisimama Yaazania, mwana wa Shafani; kila mmoja ana chetezo mkononi mwake, na harufu ya moshi wa uvumba ilipaa juu. 12 Kisha akaniambia, Mwanadamu, umeyaona wanayotenda wazee wa nyumba ya Israeli gizani, kila mtu ndani ya vyumba vyake vya sanamu? Maana husema, Bwana hatuoni; Bwana ameiacha nchi hii. 13 Akaniambia tena, Utaona tena machukizo makubwa mengine wanayoyatenda. 14 Ndipo akanileta mpaka mlango wa kuingilia katika nyumba ya Bwana, ulioelekea upande wa kaskazini, na tazama, wanawake wameketi wakimlilia Tamuzi. 15 Akaniambia, Mwanadamu umeyaona haya? Utaona tena machukizo makubwa kuliko hayo. 16 Akanileta mpaka ua wa ndani wa nyumba ya Bwana, na tazama, mlangoni pa hekalu la Bwana, kati ya ukumbi na madhabahu, walikuwako watu kama ishirini na watano, wamelipa kisogo hekalu la Bwana, na nyuso zao zimeelekea upande wa mashariki, nao wanaliabudu jua, kwa kuuelekea upande wa mashariki. 17 Basi, akaniambia, Umeyaona haya, Ee mwanadamu? Je! Ni jambo dogo sana kwa nyumba ya Yuda, wayafanye machukizo wanayoyafanya hapa? Kwa maana wameijaza nchi hii udhalimu, tena wamerejea nyuma ili kunikasirisha; na, tazama, wanaliweka tawi puani. 18 Kwa sababu hiyo mimi nami nitatenda kwa ghadhabu; jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma, na wajapolia masikioni mwangu kwa sauti kuu, sitawasikiliza.

Ezekieli 9

1 Kisha akalia kwa sauti kuu masikioni mwangu, akisema, Waamuru wale wanaousimamia mji wakaribie, kila mmoja na awe na kitu chake cha kuangamiza mkononi mwake. 2 Na tazama, watu sita wakaja, wakitokea kwa njia ya lango la juu, lielekealo upande wa kaskazini, kila mmoja ana kitu chake cha kufisha mkononi mwake; na mtu mmoja kati yao amevaa bafta, naye ana kidau cha wino cha mwandishi kiunoni. Wakaingia, wakasimama karibu na madhabahu ya shaba. 3 Na huo utukufu wa Bwana wa Israeli ulikuwa umepanda juu kutoka kwa kerubi, ambaye ulikuwa juu yake, mpaka kizingiti cha nyumba; akamwita mtu yule aliyekuwa amevaa bafta, mwenye kidau cha wino cha mwandishi kiunoni. 4 Bwana akamwambia, Pita kati ya mji, kati ya Yerusalemu, ukatie alama katika vipaji vya nyuso vya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika kati yake. 5 Na hao wengine aliwaambia, nami nalisikia, Piteni kati ya mji nyuma yake, mkapige; jicho lenu lisiachilie, wala msione huruma; 6 Waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama; tena anzeni katika patakatifu pangu. Basi, wakaanza kwa wazee waliokuwa mbele ya nyumba. 7 Akawaambia, itieni nyumba unajisi, mkazijaze nyua mizoga ya hao waliouawa; haya, enendeni. Wakaenenda, wakapiga-piga katika mji. 8 Tena ikawa, walipokuwa wakipiga, nami nikiachwa, nalianguka kifudifudi, nikalia, nikasema, Ee Bwana MUNGU! Utaangamiza mabaki yote ya Israeli, wakati wa kumwaga ghadhabu yako juu ya Yerusalemu? 9 Ndipo akaniambia, Uovu wa nyumba ya Israeli na Yuda ni mwingi sana, nayo nchi imejaa damu, nao mji umejaa kupotosha hukumu; maana husema, Bwana ameiacha nchi hii, naye Bwana haoni. 10 Nami, jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma; lakini nitaleta njia yao juu ya vichwa vyao. 11 Na tazama, mtu yule aliyevaa bafta, mwenye kidau cha wino kiunoni, akaleta habari, akisema, Nimefanya kama ulivyoniamuru.

Ezekieli 10

1 Ndipo nikaangalia, na tazama, katika anga lililokuwa juu ya vichwa vya makerubi, kulionekana juu yao kana kwamba ni yakuti samawi, kuonekana kama mfano wa kiti cha enzi. 2 Naye akamwambia mtu yule aliyevaa bafta, akasema, Ingia kati ya magurudumu yazungukayo, yaani, chini ya kerubi, ukaijaze mikono yako yote miwili makaa ya moto, toka katikati ya makerubi, ukayamwage juu ya mji. Akaingia ndani mbele ya macho yangu. 3 Basi, makerubi walisimama upande wa kuume wa nyumba, hapo alipoingia mtu yule; nalo wingu likaujaza ua wa ndani. 4 Utukufu wa Bwana ukapaa kutoka kwa kerubi yule, ukasimama juu ya kizingiti cha nyumba; nayo nyumba ikajazwa na lile wingu, na ua ulikuwa umejaa mwangaza wa utukufu wa Bwana. 5 Na sauti ya mabawa ya makerubi ikasikiwa, hata katika ua wa nje, kama sauti ya Mungu Mwenyezi, asemapo. 6 Ikawa, hapo alipomwagiza huyo mtu aliyevaa bafta, akisema, Twaa moto kutoka katikati ya magurudumu yazungukayo katikati ya hao makerubi, akaingia, akasimama karibu na gurudumu moja. 7 Na kerubi yule akanyosha mkono wake toka katikati ya makerubi, kwa moto ule uliokuwa katikati ya makerubi, akatwaa baadhi ya moto ule, akautia katika mikono ya mtu yule aliyevaa bafta; naye akautwaa, akatoka. 8 Kukaonekana katika makerubi mfano wa mkono wa mwanadamu chini ya mabawa yao. 9 Nami nikaangalia, na tazama, yalikuwako magurudumu manne karibu na makerubi, gurudumu moja karibu na kerubi mmoja, na gurudumu lingine karibu na kerubi mwingine; na kuonekana kwa magurudumu kulikuwa kana kwamba ni zabarajadi. 10 Na kuonekana kwake, yote manne yalikuwa na mfano mmoja, kana kwamba gurudumu moja lilikuwa ndani ya gurudumu lingine. 11 Walipokwenda, walikwenda kwa pande zao nne; hawakugeuka walipokwenda, lakini walifuata mpaka mahali pale kilipopaelekea kichwa; hawakugeuka walipokwenda. 12 Na mwili wao mzima, na maungo yao, na mikono yao, na mabawa yao, na magurudumu, wamejaa macho pande zote, hata magurudumu waliyokuwa nayo wale wanne. 13 Na magurudumu hayo yaliitwa Kisulisuli, nami nalisikia. 14 Kila mmoja alikuwa na nyuso nne; uso wa kwanza ulikuwa uso wa kerubi, na uso wa pili ulikuwa uso wa mwanadamu, na uso wa tatu ulikuwa uso wa simba, na uso wa nne ulikuwa uso wa tai. 15 Makerubi wakapaa juu; huyo ndiye kiumbe hai niliyemwona karibu na mto Kebari. 16 Na makerubi walipokwenda, magurudumu yale yalikwenda kando yao; na makerubi walipoinua mabawa yao, wapate kupaa juu kutoka katika dunia, magurudumu yale hayakugeuka wala kutoka kando yao. 17 Waliposimama hao, hayo nayo yalisimama; na walipopaa juu hao, hayo nayo yalipaa juu pamoja nao; maana roho ya huyo kiumbe hai ilikuwa ndani yao. 18 Kisha huo utukufu wa Bwana ukatoka pale juu ya kizingiti cha nyumba, ukasimama juu ya makerubi. 19 Nao makerubi wakainua mabawa yao, wakapaa juu kutoka katika dunia machoni pangu, hapo walipotoka nje, nayo magurudumu yakawa kando yao; wakasimama mahali pa kuingilia pa mlango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Bwana; na utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao. 20 Huyu ndiye kiumbe hai niliyemwona, chini ya Mungu wa Israeli, karibu na mto Kebari; nikajua ya kuwa hao ni makerubi. 21 Kila mmoja alikuwa na nyuso nne, na kila mmoja alikuwa na mabawa manne; na mifano ya mikono ya mwanadamu ilikuwa chini ya mabawa yao. 22 Na mfano wa nyuso zao, ni nyuso zile zile nilizoziona karibu na mto Kebari; kuonekana kwao, na wao wenyewe; kila mmoja walikwenda mbele moja kwa moja.

Ezekieli 11

1 Tena roho ikaniinua, ikanileta hata lango la upande wa mashariki wa nyumba ya Bwana, lililoelekea upande wa mashariki; na tazama, mahali pa kuingilia pa lango walikuwako watu ishirini na watano; na katikati yao nikamwona Yaazania, mwana wa Azuri, na Pelatia, mwana wa Benaya, nao ni wakuu wa watu. 2 Akaniambia, Mwanadamu, hawa ndio watu wale watungao uovu, na kutoa mashauri mabaya ndani ya mji huu; 3 wasemao, Wakati wa kujenga nyumba si karibu; mji huu ni sufuria na sisi ni nyama. 4 Basi toa unabii juu yao, Ee mwanadamu, toa unabii. 5 Roho ya Bwana ikaniangukia, naye akaniambia, Nena, Bwana asema hivi; Mmesema maneno hayo, Enyi nyumba ya Israeli; maana mimi nayajua yaingiayo katika mioyo yenu. 6 Mmewaongeza watu wenu waliouawa ndani ya mji wenu, nanyi mmezijaza njia kuu zake waliouawa. 7 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Watu wenu waliouawa, ambao mmewalaza katikati yake, hao ndio nyama hiyo, na mji huu ndio sufuria; lakini ninyi mtatolewa nje kutoka katikati yake. 8 Ninyi mmeuogopa upanga; nami nitauleta upanga juu yenu, asema Bwana MUNGU. 9 Nami nitawatoa ninyi nje kutoka katikati yake, na kuwatia katika mikono ya wageni, nami nitafanya hukumu kati yenu. 10 Mtaanguka kwa upanga; nitawahukumu katika mpaka wa Israeli; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 11 Mji huu hautakuwa sufuria lenu, wala ninyi hamtakuwa nyama ndani yake; nitawahukumu katika mpaka wa Israeli; 12 nanyi mtajua ya kuwa mimi ni Bwana; kwa maana hamuendi katika amri zangu, wala hamkuzishika hukumu zangu, bali mmetenda mambo kama hukumu za mataifa wanaowazunguka. 13 Ikawa, nilipotoa unabii, Pelatia, mwana wa Benaya, akafa. Ndipo nikaanguka kifudifudi, nikalia kwa sauti kuu, nikasema, Ee Bwana MUNGU, je! Utawakomesha kabisa mabaki ya Israeli? 14 Neno la Bwana likanijia, kusema, 15 Mwanadamu, ndugu zako, naam, ndugu zako, watu wa jamaa zako, na nyumba yote ya Israeli, wote pia, ndio hao ambao wenyeji wa Yerusalemu wamewaambia, Jitengeni mbali na Bwana, nchi hii tumepewa sisi, iwe milki yetu; 16 basi nena, Bwana MUNGU asema hivi, Ikiwa mimi nimewahamisha, wakae katika mataifa, na ikiwa mimi nimewatawanya katika nchi kadha wa kadha, pamoja na hayo nitakuwa patakatifu kwao kwa muda mchache, katika nchi zile walizozifikilia. 17 Basi nena, Bwana MUNGU asema hivi; Nitawakusanya ninyi toka kati ya kabila za watu, na kuwakutanisha toka nchi zile mlizotawanyika, nami nitawapeni nchi ya Israeli. 18 Nao watafika huko, nao wataondolea mbali vitu vyake vyote vichukizavyo, na machukizo yake yote. 19 Nami nitawapa moyo mmoja, nami nitatia roho mpya ndani yao; nami nitauondoa moyo wa kijiwe katika miili yao, nami nitawapa moyo wa nyama; 20 ili waende katika amri zangu, na kuyashika maagizo yangu, na kuyatenda; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao. 21 Bali wao ambao mioyo yao huenda kwa kuufuata moyo wa vitu vyao vichukizavyo, na machukizo yao, nitaileta njia yao iwajilie juu ya vichwa vyao, asema Bwana MUNGU. 22 Ndipo hao makerubi wakainua mabawa yao, nayo magurudumu yalikuwa karibu nao, nao utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao. 23 Utukufu wa Bwana ukapaa juu toka katikati ya mji, ukasimama juu ya mlima wa upande wa mashariki wa mji. 24 Na roho hiyo ikaniinua, ikanichukua katika maono, kwa nguvu za roho ya Mungu, hata Ukaldayo, kwa watu wale wa uhamisho. Basi maono niliyoyaona yakaniacha. 25 Ndipo nikawaambia watu wa uhamisho habari ya mambo yote aliyonionyesha Bwana.

Ezekieli 12

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Mwanadamu, wewe unakaa kati ya nyumba iliyoasi, watu ambao wana macho ya kuona, ila hawaoni, wana masikio ya kusikia, ila hawasikii; kwa maana ni nyumba iliyoasi. 3 Basi, mwanadamu, funga tayari vyombo kwa uhamisho, ukahame wakati wa mchana mbele ya macho yao; nawe utahama toka mahali pako hapa mpaka mahali pengine mbele ya macho yao; labda watafahamu, wajapokuwa ni nyumba iliyoasi. 4 Nawe utatoa vyombo vyako, wakati wa mchana, mbele ya macho yao, kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa; nawe mwenyewe utatoka, wakati wa jioni, mbele ya macho yao, kama watu watokavyo katika kuhamishwa. 5 Toboa mahali ukutani mbele ya macho yao, ukachukue vitu kwa kuvipitisha pale. 6 Mbele ya macho yao utajitwika begani pako, na kuvichukua nje gizani; utafunika uso wako, hata usiione nchi; kwa maana nimekuweka uwe ishara kwa nyumba ya Israeli. 7 Nikafanya vile vile kama nilivyoamriwa; nalitoa vyombo vyangu wakati wa mchana kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa, na wakati wa jioni nikautoboa ukuta kwa mkono wangu; nikavitoa gizani, nikavichukua begani, mbele ya macho yao. 8 Asubuhi neno la Bwana likanijia, kusema, 9 Mwanadamu, nyumba ya Israeli, je! Nyumba ile iliyoasi, hawakukuambia, Unafanya nini wewe? 10 Waambie, Bwana MUNGU asema hivi; Ufunuo huu wamhusu mkuu wa Yerusalemu, na nyumba yote ya Israeli walio kati yao. 11 Sema, Mimi ni ishara kwenu; kama mimi nilivyotenda, wao nao watatendwa vile vile; watahamishwa, watakwenda kufungwa. 12 Naye mkuu aliye kati yao atachukua begani katika giza; naye atatoka kwenda zake; watatoboa mahali ukutani, wapate kuvichukua vyombo vyao nje; atafunika uso wake, kwa sababu hataiona nchi kwa macho yake. 13 Tena wavu wangu nitautandika juu yake, naye atanaswa kwa mtego wangu; nami nitampeleka Babeli, mpaka nchi ya Wakaldayo; lakini hataiona, angawa atakufa huko. 14 Nami nitawatawanya kwa pepo zote wote wamzungukao ili wamsaidie, na vikosi vyake vyote; nami nitaufuta upanga nyuma yao. 15 Nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana; nitakapowatawanya kati ya mataifa, na kuwatupa-tupa katika nchi zote. 16 Lakini nitawasaza watu wachache miongoni mwao na kuwaokoa na upanga, na njaa, na tauni ili watangaze habari ya machukizo yao yote, kati ya mataifa huko waendako; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 17 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 18 Mwanadamu, ule chakula chako kwa matetemo, ukanywe maji yako kwa kutetemeka na kwa kuyatunza sana; 19 ukawaambie watu wa nchi, Bwana MUNGU asema hivi, katika habari zao wakaao Yerusalemu, na katika nchi ya Israeli; Watakula chakula chao kwa kukitunza sana, na maji yao watayanywa kwa ushangao, nchi yao iwe ukiwa, kwa kukosa vitu vyote viijazavyo, kwa sababu ya udhalimu wao wote wakaao ndani yake. 20 Na miji yote yenye watu itakuwa maganjo, nayo nchi itakuwa ukiwa; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 21 Neno la Bwana likanijia, kusema, 22 Mwanadamu, ni mithali gani hii mliyo nayo katika nchi ya Israeli, mkisema, Siku hizo zinakawia na maono yote hayatimizwi. 23 Basi uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Nitaikomesha mithali hii, wasiitumie tena kama mithali katika Israeli; lakini uwaambie, Siku hizo ni karibu, na utimilizo wa maono yote. 24 Kwa maana hayatakuwapo tena maono yo yote ya ubatili, wala ubashiri wa kujipendekeza, katika nyumba ya Israeli. 25 Maana mimi ni Bwana; mimi nitanena, na neno lile nitakalolinena litatimizwa; wala halitakawilishwa tena; maana katika siku zenu, Ewe nyumba iliyoasi, nitalinena neno hilo na kulitimiza, asema Bwana MUNGU. 26 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 27 Mwanadamu, tazama, hao wa nyumba ya Israeli husema, Maono hayo ayaonayo ni ya siku nyingi zijazo, naye anatabiri habari ya nyakati zilizo mbali sana. 28 Basi uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Maneno yangu hayatakawilishwa tena hata moja, bali neno nitakalolinena litatimizwa, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 13

1 Kisha neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, tabiri juu ya manabii wa Israeli wanaotabiri, uwaambie wanaotabiri kwa mioyo yao wenyewe, Lisikieni neno la Bwana; 3 Bwana MUNGU asema hivi; Ole wao manabii wajinga, wanaoifuata roho yao wenyewe, wala hawakuona neno lo lote! 4 Ee Israeli, manabii wako wamekuwa kama mbweha, mahali palipo ukiwa. 5 Hamkupanda kwenda mahali palipobomolewa, wala hamkuitengenezea nyumba ya Israeli boma, wapate kusimama vitani katika siku ya Bwana. 6 Wameona ubatili, na uganga wa uongo, hao wasemao, Bwana asema; lakini Bwana hakuwatuma; nao wamewatumainisha watu ya kuwa neno lile litatimizwa. 7 Je! Hamkuona maono ya bure, hamkunena mabashiri ya uongo? Nanyi mwasema, Bwana asema; ila mimi sikusema neno. 8 Basi tazama, Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu mmenena ubatili, na kuona uongo, basi, kwa sababu hiyo, mimi ni juu yenu, asema Bwana MUNGU. 9 Na mkono wangu utakuwa juu ya manabii wanaoona ubatili, na kutabiri uongo; hawatakuwa katika mashauri ya watu wangu, wala hawataandikwa katika maandiko ya nyumba ya Israeli, wala hawataingia katika nchi ya Israeli; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana MUNGU. 10 Kwa sababu hiyo, kwa sababu wameshawishi watu wangu, wakisema, Amani; wala hapana amani; na mtu mmoja ajengapo ukuta, tazama, waupaka chokaa isiyokorogwa vema; 11 basi waambie hao wanaoupaka ukuta chokaa isiyokorogwa vema, ya kwamba utaanguka; kutakuwa mvua ya kufurika; nanyi, enyi mvua ya mawe makubwa ya barafu, mtaanguka; na upepo wa dhoruba utaupasua. 12 Na huo ukuta utakapoanguka, je! Hamtaambiwa, Ku wapi kupaka kwenu mlikoupaka? 13 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Nitaupasua kwa upepo wa dhoruba, katika ghadhabu yangu; tena kutakuwa mvua ya barafu ya kufurika katika hasira yangu; na mawe makubwa ya barafu katika hasira ya kuukomesha. 14 Ndivyo nitakavyoubomoa ukuta mlioupaka chokaa isiyokorogwa vema, na kuuangusha chini, hata misingi yake itafunuliwa; nao utaanguka, nanyi mtaangamizwa katikati yake; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 15 Ndivyo nitakavyotimiza ghadhabu yangu juu ya ukuta ule, na juu yao walioupaka chokaa isiyokorogwa vema; nami nitawaambieni, Ukuta huo hauko sasa, wala wao walioupaka hawako; 16 yaani, manabii wa Israeli, watabirio habari za Yerusalemu, na kuona maono ya amani katika habari zake; wala hapana amani, asema Bwana MUNGU. 17 Na wewe, mwanadamu, kaza uso wako juu ya binti za watu wako, watabirio kwa akili zao wenyewe; ukatabiri juu yao, 18 useme, Bwana MUNGU asema hivi; Ole wao wanawake wale, washonao hirizi katika viungo vyote vya mikono, wawekao leso juu ya vichwa vya kila kimo, ili wawinde roho za watu; je! Mtaziwinda roho za watu wangu, na kuzihifadhi hai roho zenu wenyewe? 19 Nanyi mmeninajisi kati ya watu wangu, kwa ajili ya makonzi ya shayiri na vipande vya mkate, ili kuziua roho za watu ambao haiwapasi kufa, na kuzihifadhi hai roho za watu ambao haikuwapasa kuwa hai, kwa kuwaambia uongo watu wangu wasikilizao uongo. 20 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni kinyume cha hirizi zenu, ambazo kwa hizo mnaziwinda roho za watu kama ndege, nami nitazitoa katika mikono yenu kwa nguvu; nami nitaziachilia roho zile mnazoziwinda kama ndege. 21 Na leso zenu nazo nitazirarua, na kuwaokoa watu wangu katika mikono yenu, wala hawatakuwa katika mikono yenu tena kuwindwa; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 22 Kwa kuwa ninyi mmemhuzunisha moyo mwenye haki kwa uongo, ambaye mimi sikumhuzunisha; na kuitia nguvu mikono ya mtu mbaya, hata asigeuke, na kuiacha njia yake mbaya, na kuhifadhika; 23 basi, kwa sababu hiyo ninyi hamtaona tena ubatili, wala kutabiri mambo; nami nitawaokoa watu wangu katika mikono yenu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 14

1 Ndipo baadhi ya wazee wa Israeli wakanijia, wakaketi mbele yangu. 2 Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema, 3 Mwanadamu, watu hawa wametwaa vinyago vyao na kuvitia mioyoni mwao, nao wameweka kwazo la uovu wao mbele ya nyuso zao. Je! Ni laiki yangu niulizwe na wao katika neno lo lote? 4 Basi sema nao, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Kila mtu wa nyumba ya Israeli atwaaye vinyago vyake na kuvitia moyoni mwake, na kuliweka kwazo la uovu wake mbele ya uso wake, na kumwendea nabii; mimi, Bwana, nitamjibu neno lake sawasawa na wingi wa sanamu zake; 5 ili niwakamate nyumba ya Israeli kwa mioyo yao wenyewe, kwa sababu wamefarakana nami kwa vinyago vyao. 6 Kwa sababu hiyo uwaambie nyumba ya Israeli, Bwana MUNGU asema hivi; Rudini ninyi, mkageuke na kuviacha vinyago vyenu; mkageuze nyuso zenu zisielekee machukizo yenu yote. 7 Kwa maana kila mtu wa nyumba ya Israeli, au wa wageni wakaao katika Israeli, ajitengaye nami, na kuvitwaa vinyago vyake na kuvitia moyoni mwake, na kuliweka kwazo la uovu wake mbele ya uso wake, kisha kumwendea nabii, na kuniuliza neno kwa ajili ya nafsi yake; mimi, Bwana, nitamjibu, mimi mwenyewe; 8 nami nitaukaza uso wangu juu ya mtu yule, na kumfanya kuwa ajabu, awe ishara na mithali, nami nitamkatilia mbali, asiwe kati ya watu wangu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 9 Na nabii akidanganyika, na kusema neno, mimi, Bwana, nimemdanganya nabii yule, nami nitaunyosha mkono wangu juu yake, na kumwangamiza, asiwe kati ya watu wangu Israeli. 10 Nao watauchukua uovu wao; uovu wa nabii utakuwa sawasawa na uovu wake yule amwendeaye aulize neno; 11 ili nyumba ya Israeli wasipotee mbali nami, wala wasijitie unajisi tena kwa makosa yao yote; bali wawe watu wangu, nami niwe Mungu wao, asema Bwana MUNGU. 12 Neno la Bwana likanijia, kusema, 13 Mwanadamu, nchi itakapofanya dhambi na kuniasi, kwa kukosa, nikaunyosha mkono wangu juu yake, na kulivunja tegemeo la chakula chake, na kuipelekea njaa, na kukatilia mbali mwanadamu na mnyama; 14 wajapokuwa watu hawa watatu, Nuhu, na Danieli, na Ayubu, kuwamo ndani yake, wangejiokoa nafsi zao wenyewe tu kwa haki yao, asema Bwana MUNGU. 15 Nikipitisha wanyama wabaya ndani ya nchi ile, wakaiharibu hata ikawa ukiwa, mtu awaye yote asiweze kupita ndani yake, kwa sababu ya wanyama hao; 16 wajapokuwamo watu hawa watatu ndani yake, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hawataokoa wana wala binti; wao wenyewe tu wataokoka, bali nchi ile itakuwa ukiwa. 17 Au nikileta upanga juu ya nchi ile, na kusema, Upanga, pita kati ya nchi hii, hata nikawakatilia mbali na nchi hiyo wanadamu na wanyama; 18 wajapokuwamo watu hawa watatu ndani yake, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hawataokoa wana wala binti; bali wao wenyewe tu wataokoka. 19 Au nikipeleka tauni katika nchi ile, na kumwaga ghadhabu yangu juu yake, kwa damu; ili kuwakatilia mbali nayo wanadamu na wanyama; 20 wajapokuwamo ndani yake Nuhu, na Danieli, na Ayubu, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hawataokoa wana wala binti; watajiokoa nafsi zao tu kwa haki yao. 21 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Je! U zaidi sana nitakapoleta hukumu zangu nne zilizo kali juu ya Yerusalemu, yaani, upanga, na njaa, na wanyama wabaya, na tauni, niwakatilie mbali nayo wanadamu na wanyama? 22 Lakini, tazama, watasalia mabaki watakaochukuliwa nje, wana na binti; tazama, watawatokea ninyi, nanyi mtaiona njia yao na matendo yao; nanyi mtafarijika katika habari ya mabaya niliyoleta juu ya Yerusalemu, naam, katika habari ya mambo yote niliyoleta juu yake. 23 Nao watawafariji ninyi, mtakapoona njia yao na matendo yao; nanyi mtajua ya kuwa sikufanya bila sababu mambo yote niliyoutenda, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 15

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, mzabibu una sifa gani kuliko mti mwingine, au tawi la mzabibu lililokuwa kati ya miti ya msituni? 3 Je! Mti wake waweza kutwaliwa, ili kufanya kazi yo yote? Watu waweza kufanya chango kwa huo, ili kutundika chombo cho chote? 4 Tazama, watupwa motoni kwa kuni moto umeziteketeza ncha zake zote mbili, nao umeteketea katikati, je! Wafaa kwa kazi yo yote? 5 Tazama, ulipokuwa mzima, haukufaa kwa kazi yo yote; sembuse ukiisha kuliwa na moto, na kuteketea; je! Waweza kufaa kwa kazi yo yote? 6 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Kama mzabibu kati ya miti ya msituni, niliyoupa moto uwe kuni, ndivyo nitakavyowatoa wakaao Yerusalemu. 7 Nami nitaukaza uso wangu juu yao; nao watatoka motoni, lakini moto utawateketeza; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoukaza uso wangu juu yao. 8 Nami nitaifanya nchi kuwa ukiwa, kwa sababu wamekosa, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 16

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Mwanadamu, uujulishe Yerusalemu machukizo yake, 3 useme, Bwana MUNGU auambia Yerusalemu hivi; Asili yako na kuzaliwa kwako kwatoka katika nchi ya Mkanaani; Mwamori alikuwa baba yako, na mama yako alikuwa Mhiti. 4 Na katika habari za kuzaliwa kwako, siku ile uliyozaliwa, kitovu chako hakikukatwa, wala hukuoshwa kwa maji usafishwe; hukutiwa chumvi hata kidogo, wala hukutiwa katika nguo kabisa. 5 Hapana jicho lililokuhurumia, ili kukutendea lo lote la mambo hayo kwa kukuhurumia; lakini ulitupwa nje uwandani, kwa kuwa nafsi yako ilichukiwa, katika siku ile uliyozaliwa. 6 Nami nilipopita karibu nawe, nikakuona ukigaagaa katika damu yako, nalikuambia, Ujapokuwa katika damu yako, uwe hai; naam, nalikuambia, Ujapokuwa katika damu yako, uwe hai. 7 Nalikufanya kuwa maelfu-elfu, kama mimea ya mashamba, ukaongezeka, na kuzidi kuwa mkubwa, ukapata kuwa na uzuri mno; matiti yako yakaumbwa, nywele zako zikawa zimeota; lakini ulikuwa uchi, huna nguo. 8 Basi, nilipopita karibu nawe, nikakutazama; tazama, wakati wako ulikuwa wakati wa upendo; nikatandika upindo wa vazi langu juu yako, nikakufunika uchi wako; naam, nalikuapia, nikafanya agano nawe, asema Bwana MUNGU, ukawa wangu. 9 Kisha nikakuosha kwa maji; naam, nalikuosha kabisa damu yako, nikakupaka mafuta; 10 nikakuvika nguo ya taraza, nikakupa viatu vya ngozi ya pomboo, nikakufunga nguo ya kitani safi kiunoni mwako, nikakufunika kwa hariri. 11 Nikakupamba kwa mapambo pia, nikatia vikuku mikononi mwako, na mkufu shingoni mwako. 12 Nikatia hazama puani mwako, na pete masikioni mwako, na taji nzuri juu ya kichwa chako. 13 Hivyo ulipambwa kwa dhahabu na fedha; na mavazi yako yalikuwa ya kitani safi, na hariri, na kazi ya taraza; ulikula unga mzuri, na asali, na mafuta; nawe ulikuwa mzuri mno, ukafanikiwa hata kufikilia hali ya kifalme. 14 Sifa zako zikaenea kati ya mataifa kwa sababu ya uzuri wako; kwa maana ulikuwa mkamilifu, kwa sababu ya utukufu wangu niliokutia, asema Bwana MUNGU. 15 Lakini uliutumainia uzuri wako, ukafanya mambo ya kikahaba kwa sababu ya sifa zako, ukamwaga mambo yako ya kikahaba juu ya kila mtu aliyepita; ulikuwa wake. 16 Ukatwaa baadhi ya mavazi yako, ukajifanyia mahali palipoinuka, palipopambwa kwa rangi mbalimbali, ukafanya mambo ya kikahaba juu yake; mambo kama hayo hayatakuja wala hayatakuwako. 17 Pia ulivitwaa vyombo vyako vya uzuri, vya dhahabu yangu na vya fedha yangu, nilivyokupa, ukajifanyia sanamu za wanaume, ukafanya mambo ya kikahaba pamoja nazo; 18 ukatwaa nguo zako za kazi ya taraza, ukawafunika, ukaweka mafuta yangu na uvumba wangu mbele yao. 19 Mkate wangu niliokupa, unga mzuri, na mafuta, na asali, nilivyokulisha, ukaviweka mbele yao viwe harufu ya kupendeza; na ndivyo vilivyokuwa; asema Bwana MUNGU. 20 Pamoja na hayo uliwatwaa wana wako na binti zako, ulionizalia, ukawatoa sadaka kwao ili waliwe. Je! Mambo yako ya kikahaba ni kitu kidogo tu, 21 hata ukawaua watoto wangu, na kuwatoa kwa kuwapitisha motoni kwa hao? 22 Na katika machukizo yako yote, na mambo yako ya kikahaba, hukuzikumbuka siku za ujana wako, ulipokuwa uchi, huna nguo, ukawa ukigaagaa katika damu yako. 23 Tena, imekuwa baada ya uovu wako wote, (ole wako! ole wako! Asema Bwana MUNGU,) 24 ulijijengea mahali palipoinuka, ukajifanyia mahali palipoinuka katika kila njia kuu. 25 Umejenga mahali pako palipoinuka penye kichwa cha kila njia, ukaufanya uzuri wako kuwa chukizo, ukatanua miguu yako kwa kila mtu aliyepita karibu, ukaongeza mambo yako ya kikahaba. 26 Tena umezini na Wamisri, jirani zako, wakuu wa mwili; ukaongeza mambo yako ya kikahaba, ili kunikasirisha. 27 Basi, tazama, kwa ajili ya hayo nimenyosha mkono wangu juu yako, nami nimelipunguza posho lako, na kukutoa kwa mapenzi yao wanaokuchukia, binti za Wafilisti, walioyaonea haya mambo yako ya uasherati. 28 Pia umefanya mambo ya kikahaba pamoja na Waashuri, kwa sababu ulikuwa huwezi kushibishwa; naam, umefanya mambo ya kikahaba pamoja nao, wala hujashiba bado. 29 Pamoja na hayo umeongeza mambo yako ya kikahaba katika nchi ya Kanaani, mpaka Ukaldayo, wala hujashibishwa kwa hayo. 30 Jinsi moyo wako ulivyokuwa dhaifu, asema Bwana MUNGU, ikiwa unafanya mambo hayo yote, kazi ya mwanamke mzinzi, 31 apendaye kutawala watu; kwa kuwa wajijengea mahali pako pakuu penye kichwa cha kila njia, na kufanya mahali pako palipoinuka katika kila njia kuu; lakini hukuwa kama kahaba, kwa maana ulidharau kupokea ujira. 32 Mke wa mtu, aziniye! Akaribishaye wageni badala ya mumewe! 33 Watu huwapa makahaba wote zawadi, bali wewe unawapa wapenzi wako wote zawadi zako, na kuwapa rushwa ili waje kwako pande zote, kwa ajili ya mambo yako ya kikahaba. 34 Tena, katika mambo yako ya kikahaba, wewe na wanawake wengine ni mbalimbali, kwa kuwa hapana akufuataye katika mambo yako ya kikahaba; tena kwa kuwa unatoa ujira, wala hupewi ujira; basi, njia yako na njia yao ni mbalimbali. 35 Kwa sababu hiyo, Ewe kahaba, lisikie neno la Bwana; 36 Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu uchafu wako umemwagwa, na uchi wako umefunuliwa, kwa njia ya uzinzi wako pamoja na wapenzi wako; na kwa sababu ya vinyago vyote vya machukizo yako; na kwa sababu ya damu ya watoto wako, uliyowapa; 37 basi, tazama, nitawakusanya wapenzi wako wote ambao umejifurahisha pamoja nao, nao wote uliowapenda, pamoja na watu wote uliowachukia; naam, nitawakusanya juu yako pande zote, na kuwafunulia uchi wako, wapate kuuona uchi wako wote. 38 Nami nitakuhukumu, kama wahukumiwavyo wake walioolewa wazinio, na kumwaga damu, nami nitakupatiliza damu ya ghadhabu na wivu. 39 Tena nitakutia katika mikono yao, nao watapaangusha mahali pako pakuu, na kupabomoa mahali pako palipoinuka, nao watakuvua nguo zako, na kutwaa vyombo vyako vya uzuri, nao watakuacha uchi, huna nguo. 40 Tena wataleta mkutano wa watu juu yako, nao watakupiga kwa mawe, na kukuchoma kwa panga zao. 41 Nao watazipiga moto nyumba zako, na kutekeleza hukumu juu yako mbele ya wanawake wengi, nami nitakulazimisha kuacha mambo ya kikahaba, wala hutatoa ujira tena. 42 Hivyo ndivyo nitakavyoshibisha ghadhabu yangu juu yako, na wivu wangu utanitoka, nami nitatulia wala sitaona hasira tena. 43 Kwa sababu hukuzikumbuka siku za ujana wako, bali umenikasirisha kwa mambo hayo yote; basi, tazama, mimi nami nitaleta njia yako juu ya kichwa chako, asema Bwana MUNGU; wala hutafanya uasherati zaidi ya machukizo yako yote. 44 Tazama, kila mtu atumiaye mithali atatumia mithali hii kinyume chako, akisema, Kama mama ya mtu alivyo, ndivyo alivyo binti yake. 45 Wewe u binti ya mama yako, amchukiaye mume wake na watoto wake; nawe u umbu la maumbu yako, waliowachukia waume zao na watoto wao; mama yako alikuwa Mhiti, na baba yako Mwamori. 46 Na umbu lako mkubwa ni Samaria, akaaye mkono wako wa kushoto, yeye na binti zake; na umbu lako mdogo, akaaye mkono wako wa kuume, ni Sodoma na binti zake. 47 Lakini hukuenda katika njia zao, wala hukutenda sawasawa na machukizo yao; lakini kana kwamba hilo ni jambo dogo sana, ulikuwa umeharibika kuliko wao katika njia zako zote. 48 Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, Sodoma, umbu lako, yeye na binti zake, hawakutenda kama wewe ulivyotenda, wewe na binti zako. 49 Tazama, uovu wa umbu lako, Sodoma, ulikuwa huu; kiburi, na kushiba chakula, na kufanikiwa, hayo yalikuwa ndani yake na binti zake; tena hakuutia nguvu mkono wa maskini na mhitaji. 50 Nao walijivuna, wakafanya machukizo mbele zangu; kwa sababu hiyo naliwaondoa hapo nilipoyaona. 51 Samaria naye hakutenda nusu ya dhambi zako; bali wewe umeyaongeza machukizo yako zaidi ya hao, nawe umewapa haki maumbu yako kwa machukizo yako yote uliyoyatenda. 52 Wewe nawe, ichukue aibu yako mwenyewe, kwa kuwa umetoa hukumu juu ya maumbu yako; kwa dhambi zako ulizozitenda, zilizochukiza kuliko hao, wao wana haki kuliko wewe; naam, ufedheheke wewe nawe, ukaichukue aibu yako, kwa kuwa umewapa haki maumbu yako. 53 Nami nitawarudisha watu wao waliofungwa; wafungwa wa Sodoma na binti zake, na wafungwa wa Samaria na binti zake na wafungwa wako waliofungwa kati yao; 54 upate kuichukua aibu yako mwenyewe, na kutahayari, kwa sababu ya mambo yote uliyoyatenda, kwa kuwa umekuwa faraja kwao. 55 Na maumbu yako, Sodoma na binti zake, watairudia hali yao ya kwanza, na Samaria na binti zake watairudia hali yao ya kwanza, na wewe na binti zako mtairudia hali yenu ya kwanza. 56 Kwa maana umbu lako, Sodoma, hakutajwa kwa kinywa chako katika siku ya kiburi chako; 57 kabla uovu wako haujafunuliwa bado, kama vile wakati ule walipokutukana binti za Shamu, na wale wote waliomzunguka, binti za Wafilisti wanaokudharau pande zote. 58 Umeuchukua uasherati wako, na machukizo yako, asema Bwana. 59 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Nitakutenda vile vile kama ulivyotenda, uliyekidharau kiapo kwa kulivunja agano. 60 Walakini nitalikumbuka agano langu nililolifanya pamoja nawe, katika siku za ujana wako, nami nitaweka imara agano la milele pamoja nawe. 61 Hapo ndipo utakapozikumbuka njia zako, na kutahayarika, hapo utakapowakaribisha maumbu yako, walio wakubwa wako na wadogo wako; nami nitakupa hao wawe binti zako, lakini si kwa agano lako. 62 Nami nitaweka imara agano langu nawe; nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Bwana; 63 upate kukumbuka, na kufadhaika, usifumbue kinywa chako tena, kwa sababu ya aibu yako; hapo nitakapokusamehe yote uliyoyatenda, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 17

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, tega kitendawili, ukawaambie nyumba ya Israeli mithali; 3 useme, Bwana MUNGU asema hivi; Tai mkubwa, mwenye mabawa makubwa na manyoya marefu katika mabawa, mwenye kujaa manyoya, yaliyo ya rangi mbalimbali, alifika Lebanoni, akakitwaa kilele cha mwerezi; 4 akakikata kitawi kilicho juu katika vitawi vyake, akakichukua mpaka nchi ya biashara, akakiweka katika mji wa wachuuzi. 5 Akatwaa tena mbegu katika mbegu za nchi hiyo, akaipanda katika udongo uzaao sana, akaiweka kando ya maji mengi; aliipandikiza kama mti ukuao karibu na mto. 6 Ikakua, ikawa mzabibu wenye kuenea sana, wa kimo kifupi, ambao matawi yake yalimgeukia, na mizizi yake ilikuwa chini yake; basi ukawa mzabibu, ukatoa matawi, ukachipuza vichipuko. 7 Kulikuwa na tai mwingine mkubwa, mwenye mabawa makubwa na manyoya mengi; na tazama, mzabibu huo ukapinda mizizi yake imwelekee yeye, ukachipuza matawi yake yamwelekee yeye, toka matuta yake ulipopandwa; ili yeye apate kuunywesha. 8 Ulikuwa umepandwa katika udongo mwema, kando ya maji mengi, upate kutoa matawi, na kuzaa matunda, uwe mzabibu mzuri. 9 Basi nena wewe, Bwana MUNGU asema hivi; Je! Huo utafanikiwa? Yeye hataing'oa mizizi yake na kuyakata matunda yake, ili ukauke? Kwamba majani mabichi yake yote yachipukayo yakauke, hata ikiwa hana nguvu nyingi, wala watu wengi wa kuung'oa na mizizi yake? 10 Naam, tazama, ingawa umepandwa, je! Utafanikiwa? Hautakauka kabisa, upepo wa mashariki utakapoupiga? Naam, utakauka katika matuta hapo ulipopandwa. 11 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 12 Waambie sasa nyumba hii iliyoasi, Hamjui maana ya mambo haya? Waambie, Tazama, mfalme wa Babeli alifika Yerusalemu, akamtwaa mfalme wake, na wakuu wake, akawachukua pamoja naye mpaka Babeli; 13 akawatwaa baadhi ya wazao wa kifalme; kisha akafanya agano naye, akamwapisha; akawaondoa watu wa nchi wenye nguvu; 14 ili ufalme huo uwe duni usijiinue, lakini usimame kwa kulishika agano lake. 15 Lakini alimwasi kwa kupeleka wajumbe huko Misri, wampe farasi na watu wengi. Je! Atafanikiwa? Afanyaye mambo hayo ataokoka? Atalivunja agano, kisha akaokoka? 16 Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hakika mahali pale akaapo mfalme aliyemmilikisha, ambaye alikidharau kiapo chake, na kulivunja agano lake, ndipo atakapokufa pamoja naye kati ya Babeli. 17 Wala Farao na jeshi lake kubwa, na kusanyiko lake kuu la watu, hawatamfaa kitu vitani, watakapofanya maboma, na kujenga ngome, ili kukatilia mbali watu wengi. 18 Kwa maana amekidharau kiapo kwa kulivunja agano; na tazama, ametia mkono wake, na pamoja na hayo ameyatenda mambo hayo yote; hataokoka. 19 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Kama mimi niishivyo, hakika kiapo changu alichokidharau, na agano langu alilolivunja, nitampatiliza kichwani pake. 20 Nami nitatandika wavu wangu juu yake, naye atanaswa katika mtego wangu, nami nitamleta hata Babeli; nami nitateta naye huko kwa sababu ya kosa lake alilonikosa. 21 Na wakimbizi wake wote wa vikosi vyake vyote wataanguka kwa upanga, na hao watakaosalia watatawanyika kwenye kila upepo; nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimenena neno hili. 22 Bwana MUNGU asema hivi; Mimi nami nitakitwaa kilele kirefu cha mwerezi, na kukipandikiza mahali; na katika vitawi vyake vilivyo juu nitatwaa kitawi kimoja kilicho chororo, nami nitakipanda juu ya mlima mrefu ulioinuka sana; 23 juu ya mlima wa mahali palipoinuka pa Israeli nitakipanda; nacho kitatoa matawi, na kuzaa matunda, nao utakuwa mwerezi mzuri; na chini yake watakaa ndege wa kila namna ya mbawa; katika uvuli wa matawi yake watakaa. 24 Na miti yote ya mashamba itajua ya kuwa mimi, Bwana, nimeushusha chini mti mrefu, na kuuinua mti mfupi, na kuukausha mti mbichi, na kuusitawisha mti mkavu; mimi, Bwana, nimenena, nami nimelitenda jambo hili.

Ezekieli 18

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Je! Maana yake ni nini hata mkatumia mithali hii katika Israeli, mkisema, Baba wamekula zabibu mbichi, nao watoto wakatiwa ganzi la meno? 3 Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hamtakuwa na sababu ya kuitumia tena mithali hii katika Israeli. 4 Tazama, roho zote ni mali yangu; kama vile roho ya baba ni mali yangu, ndivyo ilivyo roho ya mwana mali yangu; roho ile itendayo dhambi itakufa. 5 Bali kama mtu ni mwenye haki, na kuyatenda yaliyo halali na haki; 6 hakula juu ya milima, wala hakuviinulia macho vinyago vya nyumba ya Israeli, wala hakumtia unajisi mke wa jirani yake, wala hakumkaribia mwanamke wakati wa kutengwa kwake; 7 wala hakumdhulumu mtu, bali amemrudishia mdeni wake rehani yake, wala hakumnyang'anya mtu mali yake kwa nguvu, naye amewapa wenye njaa chakula chake, na kuwavika nguo walio uchi; 8 ambaye hakumkopesha mtu ili apate faida, wala hakupokea ziada ya namna yo yote; naye ameuepusha mkono wake na uovu, na kufanya hukumu ya haki kati ya mtu na mwenzake; 9 tena ikiwa amezifuata sheria zangu, na kuzishika hukumu zangu; mtu huyu ni mwenye haki; hakika ataishi, asema Bwana MUNGU. 10 Walakini akizaa mwana aliye mnyang'anyi, mmwaga damu, atendaye mambo hayo mojawapo; 11 wala hakutenda mojawapo la mambo hayo yampasayo, bali amekula juu ya milima, na kumtia unajisi mke wa jirani yake, 12 na kuwadhulumu maskini na wahitaji, na kuwanyang'anya watu mali yao kwa nguvu, wala hakurudisha rehani, naye ameviinulia macho vinyago, na kufanya machukizo, 13 naye amekopesha watu ili apate faida, na kupokea ziada; je! Ataishi baada ya hayo? La, hataishi; amefanya machukizo hayo yote; hakika atakufa; damu yake itakuwa juu yake. 14 Na kama yeye huyo akizaa mwana, naye ameona dhambi zote za baba yake alizozitenda, akaogopa, asifanye neno lo lote kama hayo; 15 hakula juu ya milima, wala hakuviinulia macho vinyago vya nyumba ya Israeli, wala hakumtia unajisi mke wa jirani yake, 16 wala hakumdhulumu mtu, wala hakutwaa kitu kiwekwe rehani, wala hakumnyang'anya mtu mali yake kwa nguvu, bali amewapa wenye njaa chakula chake, na kuwafunika nguo walio uchi; 17 tena ikiwa ameuzuia mkono wake asimwonee maskini, wala hakupokea faida na ziada, naye amezifanya hukumu zangu, na kuzifuata sheria zangu; hatakufa huyu kwa sababu ya uovu wa baba yake, hakika ataishi. 18 Kwa habari za yule baba yake, kwa sababu aliwaonea watu kwa ukali mwingi, na kumnyang'anya ndugu yake mali yake kwa nguvu; na kuyatenda yasiyo mema kati ya watu wake, tazama, atakufa katika uovu wake. 19 Lakini ninyi mwasema, Kwani yule mwana asiuchukue uovu wa baba yake? Yule mwana atakapofanya yaliyo halali na haki, na kuzishika amri zangu na kuzitenda, hakika ataishi. 20 Roho itendayo dhambi, ndiyo itakayokufa; mwana hatauchukua uovu wa baba yake, wala baba hatauchukua uovu wa mwanawe, haki yake mwenye haki itakuwa juu yake, na uovu wake mwenye uovu utakuwa juu yake. 21 Lakini mtu mbaya akighairi, na kuacha dhambi zake zote alizozitenda, na kuzishika amri zangu zote, na kutenda yaliyo halali na haki, hakika ataishi, hatakufa. 22 Dhambi zake zote alizozitenda hazitakumbukwa juu yake hata mojawapo; katika haki yake aliyoitenda ataishi. 23 Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? Asema Bwana MUNGU; si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi? 24 Bali mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, na kufanya machukizo yote kama yale afanyayo mtu mwovu, je, ataishi? Katika matendo yake yote ya haki aliyoyatenda halitakumbukwa hata mojawapo. Katika kosa lile alilolikosa, naam, katika dhambi yake aliyoitenda, atakufa. 25 Lakini ninyi mwasema, Njia ya Bwana si sawa. Sikilizeni sasa, Enyi nyumba ya Israeli; Je! Njia yangu siyo iliyo sawa? Njia zenu sizo zisizo sawa? 26 Mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, akafa katika uovu huo; katika uovu wake alioutenda atakufa. 27 Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. 28 Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa. 29 Lakini nyumba ya Israeli husema, Njia ya Bwana si sawa. Ee nyumba ya Israeli, je! Njia zangu sizo zilizo sawa? Njia zenu sizo zisizo sawa? 30 Basi, nitawahukumu ninyi, nyumba ya Israeli, kila mmoja kwa kadiri ya njia zake, asema Bwana MUNGU. Rudini, mkaghairi, na kuyaacha makosa yenu yote; basi hivyo uovu wenu hautakuwa uharibifu wenu. 31 Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; jifanyieni moyo mpya na roho mpya; mbona mnataka kufa, enyi nyumba ya Israeli? 32 Maana mimi sikufurahii kufa kwake afaye, asema Bwana MUNGU; basi ghairini, mkaishi.

Ezekieli 19

1 Tena uwaombolezee wakuu wa Israeli, 2 useme, Mama yako alikuwa nini? Simba mke; alijilaza kati ya simba, kati ya wana-simba aliwalisha watoto wake. 3 Akamlea mtoto mmoja katika watoto wake, akawa mwana-simba, akajifunza kuwinda mawindo, akala watu. 4 Mataifa nao wakapata habari zake, akanaswa katika rima lao, wakamchukua kwa kulabu mpaka nchi ya Misri. 5 Basi mamaye alipoona kwamba amemngoja, na tumaini lake limepotea, akatwaa mtoto mwingine katika watoto wake, akamfanya mwana-simba. 6 Naye akaenda huko na huko kati ya simba, akawa mwana-simba, akajifunza kuwinda mawindo, akala watu. 7 Akayajua majumba yao, akaiharibu miji yao; nchi ikawa ukiwa, navyo vitu vilivyoijaza, kwa sababu ya mshindo wa kunguruma kwake. 8 Ndipo mataifa wakajipanga juu yake pande zote toka nchi zote; wakaunda wavu wao juu yake; akanaswa katika rima lao. 9 Wakamtia katika tundu kwa kulabu, wakamleta kwa mfalme wa Babeli wakamtia ndani ya ngome, sauti yake isisikiwe tena juu ya milima ya Israeli. 10 Mama yako alikuwa kama mzabibu, katika damu yako, uliopandwa karibu na maji; akazaa sana na kujaa matawi, kwa sababu ya maji mengi. 11 Naye alikuwa na vijiti vya nguvu, kwa fimbo za enzi zao watawalao, na kimo chao kiliinuka kati ya matawi manene, wakaonekana kwa urefu wao, pamoja na wingi wa matawi yao. 12 Lakini aling'olewa kwa ghadhabu, akaangushwa chini, upepo wa mashariki ukakausha matunda yake; vijiti vyake vya nguvu vikavunjika, vikakauka; moto ulivila. 13 Na sasa umepandwa jangwani, katika nchi kavu, ya ukame. 14 Na moto umetoka katika vijiti vya matawi yake, umekula matunda yake, hata hana tena kijiti cha nguvu kifaacho kwa fimbo ya enzi ya kutawala. Na hayo ni maombolezo, nayo yatakuwa maombolezo.

Ezekieli 20

1 Ikawa katika mwaka wa saba, mwezi wa tano, siku ya kumi ya mwezi, baadhi ya wazee wa Israeli walikuja ili kuuliza kwa Bwana, wakaketi mbele yangu. 2 Neno la Bwana likanijia, kusema, 3 Mwanadamu, sema na wazee wa Israeli, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Je! Mmekuja kuniuliza neno? Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, sitaulizwa neno na ninyi. 4 Je! Utawahukumu, mwanadamu, utawahukumu? Uwajulishe machukizo ya baba zao; 5 uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Katika siku ile nilipochagua Israeli, na kuwainulia wazao wa nyumba ya Yakobo mkono wangu, na kujidhihirisha kwao katika nchi ya Misri, hapo nilipowainulia mkono wangu, nikisema, Mimi ni Bwana, Mungu wenu; 6 katika siku ile naliwainulia mkono wangu, kuwatoa katika nchi ya Misri, na kuwaingiza katika nchi niliyowapelelezea, ijaayo maziwa na asali, ambayo ni utukufu wa nchi zote; 7 nikawaambia, Kila mtu kwenu na atupilie mbali machukizo ya macho yake, wala msijitie unajisi kwa vinyago vya Misri, Mimi ni Bwana, Mungu wenu. 8 Lakini waliniasi, wala hawakutaka kunisikiliza; hawakutupilia mbali kila mtu machukizo ya macho yake, wala hawakuviacha vinyago vya Misri; ndipo nikasema kwamba nitamwaga ghadhabu yangu juu yao, ili kuitimiza hasira yangu juu yao, katikati ya nchi ya Misri. 9 Lakini nalitenda kwa ajili ya jina langu, ili lisitiwe unajisi mbele ya macho ya mataifa, ambao walikaa pamoja nao, ambao machoni pao nalijidhihirisha kwao, kwa kuwatoa katika nchi ya Misri. 10 Basi nikawatoa katika nchi ya Misri, nikawaleta jangwani. 11 Nikawapa amri zangu, na kuwaonyesha hukumu zangu, ambazo mwanadamu ataishi kwazo, kama akizitenda. 12 Tena naliwapa sabato zangu, ziwe ishara kati ya mimi na wao, wapate kujua ya kuwa mimi, Bwana, ndimi niwatakasaye. 13 Lakini nyumba ya Israeli waliniasi jangwani; hawakuenda katika amri zangu, wakazikataa hukumu zangu, ambazo mwanadamu ataishi kwazo, kama akizitenda; na sabato zangu walizitia unajisi sana; ndipo nikasema, Nitamwaga hasira yangu juu yao jangwani, ili niwaangamize. 14 Lakini nalitenda kwa ajili ya jina langu, lisitiwe unajisi machoni pa mataifa, ambao naliwatoa mbele ya macho yao. 15 Tena naliwainulia mkono wangu jangwani, ya kwamba sitawaingiza katika nchi ile niliyokuwa nimewapa, ijaayo maziwa na asali, ambayo ni utukufu wa nchi zote; 16 kwa sababu walizikataa hukumu zangu, wala hawakuenda katika amri zangu, wakazitia unajisi sabato zangu, kwa maana mioyo yao iliandama vinyago vyao. 17 Walakini jicho langu likawahurumia nisiwaangamize kabisa, wala sikuwakomesha kabisa jangwani. 18 Kisha nikawaambia watoto wao jangwani, Msiende katika amri za baba zenu, wala msizishike hukumu zao, wala msijitie unajisi kwa vinyago vyao. 19 Mimi ni Bwana, Mungu wenu; endeni katika amri zangu, mkazishike hukumu zangu, na kuzitenda; 20 zitakaseni sabato zangu; zitakuwa ishara kati ya mimi na ninyi, mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu. 21 Lakini watoto hao waliniasi; hawakuenda katika amri zangu, wala hawakuzishika hukumu zangu kuzitenda, ambazo mwanadamu ataishi kwazo kama akizitenda; walizitia unajisi sabato zangu, ndipo nikasema, kwamba nitamwaga ghadhabu yangu juu yao, ili kuitimiza hasira yangu juu yao jangwani. 22 Lakini naliuzuia mkono wangu, nikatenda kwa ajili ya jina langu, lisitiwe unajisi mbele ya macho ya mataifa, ambao mbele ya macho yao naliwatoa. 23 Tena naliwainulia mkono wangu jangwani, kwamba nitawatawanya kati ya mataifa, na kuwatapanya katika nchi mbalimbali; 24 kwa sababu hawakuzitekeleza hukumu zangu, bali walizikataa amri zangu, nao walizitia unajisi sabato zangu, na macho yao yaliandama vinyago vya baba zao. 25 Tena naliwapa amri zisizokuwa njema, na hukumu ambazo hawakuweza kuishi kwazo; 26 nami nikawatia unajisi kwa matoleo yao wenyewe, kwa kuwa walipitisha motoni wote waliofungua tumbo; ili kuwafanya kuwa ukiwa, wakapate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 27 Basi, mwanadamu, sema na nyumba ya Israeli, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Baba zenu wamenitukana kwa jambo hili, kwa kuwa wamekosa kosa juu yangu. 28 Kwa maana nilipokuwa nimekwisha kuwaingiza katika nchi ile, ambayo naliuinua mkono wangu kuwapa, wakati huo walipoona kila mlima mrefu, na kila mti wenye majani mengi, walitoa matoleo yao huko, na huko walitoa chukizo la sadaka zao, na huko walifanya nukato la kupendeza, na huko walimimina sadaka zao za kunywewa. 29 Ndipo nikawauliza, Nini maana yake mahali palipoinuka mnapopaendea? Basi, jina lake mahali pale ni Bama hata leo. 30 Basi, uwaambie nyumba ya Israeli, Bwana MUNGU asema hivi; Je! Mnajitia unajisi kwa kuzifuata njia za baba zenu? Mnakwenda kufanya uasherati kwa kuyafuata machukizo yao? 31 Tena mtoapo matoleo yenu, na kuwapitisha watoto wenu motoni, je! Mnajitia unajisi kwa vinyago vyenu vyote hata leo? Na mimi je! Niulizwe neno nanyi, Enyi nyumba ya Israeli? Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, sitaulizwa neno na ninyi. 32 Na haya yote yaingiayo katika nia zenu hayatakuwa kamwe; ikiwa mmesema, Sisi tutakuwa sawasawa na mataifa, sawasawa na jamaa za nchi nyingine, kutumikia miti na mawe. 33 Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hakika kwa mkono hodari, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa ghadhabu iliyomwagika, nitakuwa mfalme juu yenu; 34 nami nitawatoa katika mataifa, na kuwakusanya, na kuwatoa katika nchi mlizotawanyika ndani yake, kwa mkono hodari, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa ghadhabu iliyomwagika; 35 nami nitawaingiza katika jangwa la mataifa, na huko ndiko nitakakoteta nanyi uso kwa uso. 36 Kama nilivyoteta na baba zenu katika jangwa la Misri, ndivyo nitakavyoteta nanyi, asema Bwana MUNGU. 37 Nami nitawapitisha chini ya fimbo, nami nitawaingiza katika mafungo ya agano. 38 Nami nitawasafisha kwa kuwatoa waasi, na hao walionikosa; nitawatoa katika nchi wanayokaa ugenini, lakini hawataingia katika nchi ya Israeli; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 39 Na katika habari zenu, enyi nyumba ya Israeli, Bwana MUNGU asema hivi, Enendeni, mkavitumikie vinyago vyenu kila mmoja wenu; na wakati wa baadaye pia, kama hamtaki kunisikiliza; lakini jina langu takatifu hamtalitia unajisi tena, kwa matoleo yenu, na kwa vinyago wenu. 40 Kwa maana katika mlima wangu mtakatifu, katika mlima mrefu sana wa Israeli, asema Bwana MUNGU, ndiko watakakonitumikia nyumba yote ya Israeli, wote pia katika nchi ile; nami nitawatakabali huko, na huko nitataka matoleo yenu, na malimbuko ya dhabihu zenu, pamoja na vitu vyenu vitakatifu vyote. 41 Nitawatakabali kama harufu ipendezayo, nitakapowatoa katika mataifa, na kuwakusanya toka nchi zile mlizotawanyika; nami nitatakaswa kwenu machoni pa mataifa. 42 Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapowaingiza katika nchi ya Israeli, katika nchi ile ambayo niliuinua mkono wangu kwamba nitawapa baba zenu. 43 Na huko mtazikumbuka njia zenu, na matendo yenu yote, ambayo mmejitia unajisi kwayo; nanyi mtajichukia katika macho yenu wenyewe, kwa sababu ya maovu yenu yote mliyoyatenda. 44 Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapokuwa nimetenda nanyi kwa ajili ya jina langu, si sawasawa na njia zenu mbaya, wala si sawasawa na matendo yenu mabovu, enyi nyumba ya Israeli, asema Bwana MUNGU. 45 Neno la Bwana likanijia, kusema, 46 Mwanadamu, uelekeze uso wako kusini, ukadondoze neno lako upande wa kusini, ukatabiri juu ya msitu wa uwanda wa Negebu, 47 ukauambie msitu wa Negebu, Lisikie neno la Bwana; Bwana MUNGU asema hivi; Tazama nitawasha moto ndani yako, nao utakula kila mti mbichi ndani yako, na kila mti mkavu; miali ya moto ule haitazimika, na nyuso zote toka kusini hata kaskazini zitateketezwa kwa moto huo. 48 Na watu wote wenye mwili wataona ya kuwa mimi, Bwana, nimeuwasha; hautazimika. 49 Ndipo nikasema, Ee Bwana MUNGU, wao hunisema; Je! Mtu huyu si mtu mwenye kupiga mithali?

Ezekieli 21

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, uelekeze uso wako kuelekea Yerusalemu, ukadondoze neno lako upande wa mahali patakatifu, ukatabiri juu ya nchi ya Israeli; 3 uiambie nchi ya Israeli, Bwana asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, nami nitautoa upanga wangu alani, nami nitamkatilia mbali nawe mtu mwenye haki na mtu mbaya. 4 Basi, kwa kuwa nitamkatilia mbali nawe mtu mwenye haki na mtu mbaya, upanga wangu utatoka alani mwake, uwe juu ya watu wote wenye mwili toka kusini hata kaskazini, 5 na watu wote wenye mwili watajua ya kuwa mimi, Bwana, nimeufuta upanga wangu alani mwake; hautarudi tena. 6 Ugua, basi, Ee mwanadamu; kwa kuvunjika kwake viuno vyako, na kwa uchungu, utaugua mbele ya macho yao. 7 Na itakuwa, wakuambiapo, Mbona unaugua? Ndipo utakaposema, Kwa sababu ya habari hizo, maana linakuja; na kila moyo utayeyuka, na mikono yote itakuwa dhaifu, na kila roho itazimia, na magoti yote yatalegea kama maji; tazama, linakuja, nalo litatendeka, asema Bwana MUNGU. 8 Neno la Bwana likanijia, kusema, 9 Mwanadamu, tabiri, useme, Bwana asema hivi; Nena, Upanga, upanga, umenolewa na kusuguliwa, 10 umenolewa ili kufanya machinjo; umesuguliwa ili uwe kama umeme; basi je! Tufanye furaha? Upanga unadharau fimbo ya mwanangu, kama unavyodharau kila mti. 11 Nao umenolewa usuguliwe, upate kushikwa mkononi; upanga umenolewa, naam, umesuguliwa, ili kutiwa katika mkono wake auaye. 12 Piga kelele, utoe sauti ya uchungu, Ee mwanadamu, kwa maana upanga u juu ya watu wangu, u juu ya wakuu wote wa Israeli; wametolewa wauawe na upanga pamoja na watu wangu, basi, jipige pajani. 13 Kwa maana kuna kujaribiwa; itakuwaje, basi, ikiwa upanga unaidharau hiyo fimbo? Haitakuwapo tena; asema Bwana MUNGU. 14 Basi, wewe mwanadamu, tabiri, ukapige makofi; upanga huo na uongezwe mara mbili, hata mara tatu; upanga wao waliotiwa jeraha kiasi cha kuwaua; ni upanga wa mkuu aliyetiwa jeraha kiasi cha kumwua; uwazungukao pande zote. 15 Nimeweka ncha ya upanga huo juu ya malango yao yote, ili mioyo yao iyeyuke, yakaongezeke makwazo yao; aha! Umefanywa kuwa kama umeme, umenolewa, ili uchinje. 16 Jiweke tayari, enenda upande wa kuume; jipange, enenda upande wa kushoto; mahali po pote utakapouelekeza uso wako. 17 Mimi nami nitapiga makofi, mimi nami nitashibisha ghadhabu yangu; mimi, Bwana, nimenena neno hili. 18 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 19 Tena, mwanadamu, ujiwekee njia mbili, upanga wa mfalme wa Babeli upate kuja; hizo mbili zitatoka katika nchi moja; ukaandike mahali, upaandike penye kichwa cha njia iendayo mjini. 20 Utaagiza njia, upanga upate kufikilia Raba wa wana wa Amoni, na kufikilia Yuda katika Yerusalemu, wenye maboma. 21 Maana mfalme wa Babeli alisimama penye njia panda, penye kichwa cha njia hizo mbili, ili atumie uganga; aliitikisa mishale huko na huko, akaziuliza terafi, akayatazama maini. 22 Katika mkono wake wa kuume alikuwa na kura ya Yerusalemu, kuviweka vyombo vya kubomolea, kufumbua kinywa katika machinjo, kuiinua sauti kwa kupiga kelele sana, kuweka vyombo vya kubomolea juu ya malango, kufanya maboma, na kujenga ngome. 23 Jambo hili litakuwa kwao kama uganga wa ubatili, mbele ya macho yao waliowaapia viapo lakini ataufanya uovu ukumbukwe, ili kwamba wakamatwe. 24 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa mmeufanya uovu wenu ukumbukwe, kwa maana makosa yenu yamefunuliwa, hata dhambi zenu zikaonekana kwa matendo yenu; kwa sababu mmekumbukwa, mtakamatwa kwa mkono. 25 Na wewe, Ewe mtu mwovu, uliyetiwa jeraha kiasi cha kukuua, mkuu wa Israeli, ambaye siku yako imekuja, katika wakati wa uovu wa mwisho; 26 Bwana MUNGU asema hivi; Kiondoe kilemba, ivue taji; haya hayatakuwa tena kama yalivyo; kikweze kilicho chini, kakishushe kilichoinuka. 27 Nitakipindua, nitakipindua, nitakipindua; hiki nacho hakitakuwa tena, hata atakapokuja yeye ambaye ni haki yake; nami nitampa. 28 Nawe, mwanadamu, tabiri useme, Bwana MUNGU asema hivi, katika habari za wana wa Amoni, na katika habari za aibu yao; Nena, Upanga; upanga umefutwa; umesuguliwa, ili kuua, ili kuufanya uue sana, upate kuwa kama umeme; 29 wakati wakuoneapo ubatili, wakati wakufanyiao uganga wa uongo, ili kukuweka juu ya shingo zao waliotiwa jeraha kiasi cha kuwaua, ambao siku yao imekuja, katika wakati wa uovu wa mwisho. 30 Uurudishe alani mwake. Mahali pale ulipoumbwa, katika nchi uliyozaliwa; nitakuhukumu wewe. 31 Nami nitamwaga ghadhabu yangu juu yako; nitakupulizia moto wa hasira yangu; nami nitakutia katika mikono ya watu walio kama hayawani, wajuao sana kuangamiza. 32 Utakuwa kuni za kutiwa motoni; damu yako itakuwa katikati ya nchi; hutakumbukwa tena; maana mimi, Bwana, nimenena neno hili.

Ezekieli 22

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Na wewe, mwanadamu, je! Utauhukumu, utauhukumu mji huu wa damu? Basi uujulishe machukizo yake yote. 3 Nawe utasema, Bwana MUNGU asema hivi; Mji umwagao damu ndani yake, ili wakati wake upate kuja; mji ufanyao vinyago juu ya nafsi yake, ili ujitie unajisi! 4 Umekuwa na hatia katika damu yako uliyomwaga, nawe umekuwa na unajisi kwa vinyago vyako ulivyovifanya; nawe umezileta karibu siku zako, nawe umefika karibu na miaka yako; basi, kwa sababu ya hayo, nimekufanya kuwa lawama kwa mataifa, na kuwa dhihaka katika nchi zote. 5 Zilizo karibu, na zilizo mbali nawe, zitakudhihaki, Ewe mchafu, uliyejaa fujo. 6 Tazama, wakuu wa Israeli, kila mmoja kwa kadiri ya nguvu zake, wamekuwamo ndani yako, ili kumwaga damu. 7 Ndani yako wamedharau baba na mama; kati yako wamewatenda wageni udhalimu; ndani yako wamewaonea yatima na mjane. 8 Umevidharau vitu vyangu vitakatifu, umezitia unajisi sabato zangu. 9 Wasingiziaji wamekuwamo ndani yako, ili kumwaga damu; na ndani yako wamekula juu ya milima; kati yako wamefanya uasherati. 10 Ndani yako wamefunua uchi wa baba zao; ndani yako wamemfanyia nguvu mwanamke asiye safi wakati wa kutengwa kwake. 11 Na mtu mmoja amefanya chukizo pamoja na mke wa jirani yake; na mtu mwingine amemharibu mke wa mwanawe kwa uasherati; na mtu mwingine ndani yako amemfanyia nguvu umbu lake, binti ya babaye. 12 Ndani yako wamepokea rushwa ili kumwaga damu; umepokea riba na faida; nawe kwa choyo umepata mapato kwa kuwadhulumu jirani zako, nawe umenisahau mimi, asema Bwana MUNGU. 13 Basi, tazama, nimeipigia kofi hiyo faida uliyopata kwa njia isiyo haki, na hiyo damu yako iliyokuwa kati yako. 14 Je! Moyo wako waweza kuvumilia, au mkono wako waweza kuwa hodari, katika siku zile nitakapokutenda mambo? Mimi, Bwana, nimenena neno hili, tena nitalitenda. 15 Nami nitakutawanya kati ya mataifa, na kukutapanya kati ya nchi mbalimbali; nami nitauteketeza uchafu wako, ili ukutoke. 16 Nawe utatiwa unajisi ndani ya nafsi yako, mbele ya macho ya mataifa; nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 17 Neno la Bwana likanijia, kusema, 18 Mwanadamu, nyumba ya Israeli imekuwa taka za fedha kwangu; wote wamekuwa shaba, na bati, na chuma, na risasi, kati ya tanuu; wamekuwa taka za fedha. 19 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu ninyi nyote mmekuwa taka za fedha, tazama, nitawakusanya kati ya Yerusalemu. 20 Kama vile watu wakusanyavyo fedha, na shaba, na chuma, na risasi, na bati, kati ya tanuu, ili kuvifukutia moto na kuviyeyusha; ndivyo nitakavyowakusanya ninyi katika hasira yangu, na ghadhabu yangu, nami nitawalaza huko, na kuwayeyusha. 21 Naam, nitawakusanya, na kuwafukutia moto wa ghadhabu yangu, nanyi mtayeyushwa kati yake. 22 Kama fedha iyeyushwavyo kati ya tanuu, ndivyo mtakavyoyeyushwa kati yake; nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimemwaga ghadhabu yangu juu yenu. 23 Neno la Bwana likanijia, kusema, 24 Mwanadamu, uiambie nchi, Wewe u nchi isiyosafika, wala kunyeshewa mvua siku ya ghadhabu. 25 Fitina ya manabii wake imo ndani yake, kama simba angurumaye akirarua mawindo; wamekula roho za watu; hutwaa kwa nguvu hazina na vitu vya thamani; wameongeza hesabu ya wajane wake ndani yake. 26 Makuhani wake wameihalifu sheria yangu, wametia unajisi vitu vyangu vitakatifu; hawakuweka tofauti ya vitu vitakatifu na vitu vya kutumiwa sikuzote; wala hawakuwafundisha watu kupambanua vitu vichafu na vitu vilivyo safi, nao wamefumba macho yao, wasiziangalie sabato zangu, nami nimetiwa unajisi kati yao. 27 Wakuu wake kati yake wamekuwa kama mbwa-mwitu wakirarua mawindo; ili kumwaga damu, na kuharibu roho za watu, wapate faida kwa njia isiyo halali. 28 Na manabii wake wamewapakia chokaa isiyokorogwa vema, wakiona ubatili, na kuwatabiria maneno ya uongo, wakisema, Bwana MUNGU asema hivi; iwapo Bwana hakusema neno. 29 Watu wa nchi wametumia udhalimu, wamenyang'anya kwa nguvu; naam, wamewatenda jeuri maskini na wahitaji, nao wamewaonea wageni bila haki. 30 Nami nikatafuta mtu miongoni mwao, atakayelitengeneza boma, na kusimama mbele zangu mahali palipobomoka, kwa ajili ya nchi, nisije nikaiharibu, lakini sikuona mtu. 31 Kwa sababu hiyo nimemwaga ghadhabu yangu juu yao; nimewateketeza kwa moto wa hasira yangu; nami nimeileta njia yao wenyewe juu ya vichwa vyao, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 23

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Mwanadamu, palikuwa na wanawake wawili, binti za mama mmoja; 3 nao walizini huko Misri; walizini wakati wa ujana wao; huko vifua vyao vililemewa, na huko waliyabana matiti ya ubikira wao. 4 Na majina yao, mkubwa aliitwa Ohola, na umbu lake Oholiba; wakawa wangu, wakazaa wana na binti. Na katika hayo majina yao, Samaria ni Ohola, na Yerusalemu ni Oholiba. 5 Na Ohola alifanya mambo ya kikahaba alipokuwa wangu; naye alipenda mno wapenzi wake, Waashuri, jirani zake, 6 waliovikwa samawi, maliwali na mawaziri, wote vijana wa kutamanika, wapanda farasi wakipanda farasi zao. 7 Akawagawia mambo yake ya kikahaba, watu wateule wa Ashuru, wote pia; akajitia unajisi kwa vinyago vyote vya kila mmoja wa hao aliowapenda. 8 Wala hakuyaacha mambo yake ya kikahaba tangu siku za Misri, kwa maana wakati wa ujana wake walilala naye, wakayabana matiti ya ubikira wake wakamwaga uzinzi wao juu yake. 9 Kwa sababu hiyo nalimtia katika mikono ya wapenzi wake, katika mikono ya Waashuri, aliowapendelea. 10 Na hawa wakaufunua uchi wake, wakatwaa wanawe na binti zake, wakamwua yeye kwa upanga; akawa jina la aibu kati ya wanawake; kwa maana walitoa hukumu juu yake. 11 Na umbu lake, Oholiba, akayaona hayo walakini alizidi kuharibika kuliko yeye, kwa kupendelea kwake, na kwa uzinzi wake, uliokuwa mwingi kuliko uzinzi wa umbu lake. 12 Aliwapendelea Waashuri, maliwali na mawaziri, jirani zake, waliovikwa nguo za shani, wapanda farasi wakipanda farasi zao, wote pia vijana wa kutamanika. 13 Nikaona ya kuwa ametiwa unajisi; wote wawili walifuata njia moja. 14 Naye akaongeza uzinzi wake; kwa maana aliona watu waume, ambao sura zao zimeandikwa ukutani, sura za Wakaldayo zilizoandikwa kwa rangi nyekundu; 15 waliofungiwa mikumbuu viunoni mwao, na vilemba vilivyotiwa rangi vichwani mwao; wote wakuu wa kuangaliwa, kwa mfano wa wana wa Babeli katika Ukaldayo, katika nchi ya kuzaliwa kwao. 16 Na mara alipowaona aliwapendelea, akatuma wajumbe kwao hata Ukaldayo. 17 Na watu wa Babeli wakamwendea katika kitanda cha mapenzi, wakamtia unajisi kwa uzinzi wao, akatiwa unajisi nao, kisha roho yake ikafarakana nao. 18 Basi alifunua uzinzi wake, na kufunua uchi wake; ndipo roho yangu ikafarakana naye, kama ilivyofarakana na umbu lake. 19 Lakini aliongeza uzinzi wake, akikumbuka siku za ujana wake, alipofanya mambo ya kikahaba katika nchi ya Misri. 20 Akawapendelea wapenzi wao, ambao nyama ya mwili wao ni kama nyama ya mwili wa punda, nacho kiwatokacho ni kama kiwatokacho farasi. 21 Ndivyo ulivyokumbuka uasherati wa ujana wako, yalipobanwa matiti yako na Wamisri, kwa maziwa ya ujana wako. 22 Kwa sababu hiyo, Ewe Oholiba, Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, nitawainua wapenzi wako juu yako, ambao roho yako imefarakana nao, nami nitawaleta juu yako pande zote; 23 watu wa Babeli, na Wakaldayo wote, Pekodi na Shoa na Koa, na Waashuri wote pamoja nao; vijana wa kutamanika, wote pia, maliwali na mawaziri, wakuu, na watu wenye sifa, wote wenye kupanda farasi. 24 Nao watakuja kwako na silaha zao, na magari ya vita, na magurudumu, na wingi wa mataifa; watajipanga juu yako kwa ngao, na vigao, na chapeo za shaba, pande zote; nami nitawapa uwezo wa kuhukumu, nao watakuhukumu sawasawa na hukumu zao. 25 Nami nitaweka wivu wangu juu yako, nao watakutenda mambo kwa ghadhabu; watakuondolea pua yako na masikio yako; na mabaki yako wataanguka kwa, upanga; watawatwaa wanao na binti zako; na mabaki yako watateketea motoni. 26 Pia watakuvua nguo zako, na kukuondolea vyombo vyako vya uzuri. 27 Hivyo ndivyo nitakavyoukomesha uasherati wako, na uzinzi wako, ulioletwa toka nchi ya Misri; usije ukawainulia macho yako, na kukumbuka Misri tena. 28 Maana Bwana MUNGU asema hivi, Tazama nitakutia katika mikono yao unaowachukia, katika mikono yao, ambao roho imefarakana nao; 29 nao watakutenda mambo kwa chuki, watakuondolea kazi zako zote, watakuacha uchi, huna nguo na aibu ya mambo yako ya kikahaba itafunuliwa, uasherati wako na uzinzi wako. 30 Utatendwa mambo hayo kwa sababu umezini na hao wasioamini, na kwa sababu umetiwa unajisi kwa vinyago vyao. 31 Umekwenda katika njia ya umbu lako; basi nitatia kikombe chake katika mkono wako. 32 Bwana MUNGU asema hivi; Utakinywea kikombe cha umbu lako; chenye nafasi nyingi kikubwa; utadhihakiwa na kudharauliwa; kimejaa sana. 33 Utajazwa ulevi na sikitiko, kwa kikombe cha ushangao na ukiwa, kikombe cha umbu lako Samaria. 34 Naam, utakinywea hata hakitabaki kitu ndani yake, utavitafuna vigae vyake, utayararua maziwa yako; maana mimi, Bwana MUNGU, nimenena neno hili. 35 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa umenisahau, na kunitupa nyuma yako, basi kwa hiyo, uchukue uasherati wako na uzinzi wako. 36 Tena Bwana akaniambia, Mwanadamu, utawahukumu Ohola na Oholiba? Basi uwahubiri machukizo yao. 37 Maana wamezini, na damu imo mikononi mwao, nao wamezini na vinyago vyao; tena wana wao walionizalia wamewapitisha katika moto ili waliwe nao. 38 Tena wamenitenda haya; wamepatia unajisi mahali pangu patakatifu, siku ile ile, nao wamezitangua sabato zangu. 39 Kwa maana walipokuwa wamekwisha kuvichinjia vinyago vyao watoto wao, ndipo walipoingia patakatifu pangu, siku ile ile, wapatie unajisi, na tazama, wamefanya hivyo kati ya nyumba yangu. 40 Tena mmewatuma watu kuwaita watokao mbali; ambao mjumbe alitumwa kwao, na tazama, wakaja; nawe ulijiosha kwa ajili yao, ulitia rangi macho yako, na kujipamba vyombo vya uzuri; 41 ukaketi juu ya kitanda cha enzi, na meza imeandikwa tayari mbele yake, ambayo juu yake uliweka uvumba wangu na mafuta yangu. 42 Na sauti za wingi wa watu wenye hali ya raha zilikuwa pamoja naye; na pamoja na watu wasio na adabu, waliletwa walevi toka jangwani; wakawatia vikuku mikononi, na taji nzuri juu ya vichwa vyao. 43 Ndipo nikasema, Huyo aliye mkongwe atafanya uzinzi! Sasa hao watazini naye, naam, na yeye! 44 Wakamwingilia kama watu wamwingiliavyo kahaba; ndivyo walivyowaingilia Ohola na Oholiba, wanawake wale waasherati. 45 Basi watu wenye haki watawahukumu, kwa hukumu iwapasayo wazinzi, na kwa hukumu iwapasayo wanawake wamwagao damu; kwa sababu wao ndio wazinzi, na mikononi mwao mna damu. 46 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Nitaleta kusanyiko la watu juu yao, nami nitawatoa warushwe huko na huko, na kutekwa nyara. 47 Na kusanyiko hilo watawapiga kwa mawe, na kuwaua kwa panga zao; watawaua wana wao na binti zao, na kuziteketeza nyumba zao kwa moto. 48 Hivyo nitaukomesha uasherati katika nchi hii, ili wanawake wote wafundishwe, wasifanye mambo ya uasherati wenu. 49 Nao watawalipa ninyi malipo ya uasherati wenu, nanyi mtachukua dhambi za vinyago vyenu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana MUNGU.

Ezekieli 24

1 Tena, katika mwaka wa kenda, mwezi wa kumi, siku ya kumi ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, liandike jina la siku hii, naam, la siku ii hii; mfalme wa Babeli ameukaribia Yerusalemu siku iyo hiyo. 3 Ukawatungie mithali nyumba ya kuasi, ukawaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Teleka sufuria, liteleke; ukatie maji ndani yake; 4 vikusanye vipande vyake ndani yake, naam, kila kipande chema, paja na bega; lijaze mifupa iliyochaguliwa. 5 Uwatwae wateule wa kundi la kondoo, ukafanye chungu ya mifupa chini yake; ukalitokose sana; naam, mifupa yake itokoswe ndani yake. 6 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Ole wake mji wa damu! Hilo sufuria ambalo kutu yake i ndani yake, ambalo kutu yake haikulitoka; litoe kipande kipande; hapana kura iliyoanguka juu yake. 7 Maana damu yake imo ndani yake; aliiweka juu ya jabali lililo wazi; hakuimwaga juu ya nchi, apate kuifunika kwa mavumbi; 8 ili ipandishe ghadhabu ya kulipa kisasi, nimeiweka damu yake juu ya jabali lililo wazi, isipate kufunikwa. 9 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Ole wake mji wa damu! Mimi nami nitaiongeza chungu. 10 Tia kuni nyingi, uchochee moto, itokose nyama sana, fanyiza mchuzi mzito, mifupa ikateketee. 11 Kisha litie juu ya makaa yake, tupu, lipate moto, na shaba yake iteketee, uchafu wake uyeyushwe, na kutu yake iteketee. 12 Amejidhoofisha kwa taabu, lakini kutu yake nyingi haikumtoka; kutu yake haitoki kwa moto. 13 Katika uchafu wako mna uasherati, kwa maana nimekusafisha, ila wewe hukusafika; hutasafishwa tena uchafu wako ukutoke, hata nitakapokuwa nimeituliza hasira yangu kwako. 14 Mimi, Bwana, nimenena neno hili, nalo litakuwa; nami nitalifanya; sitaachilia, wala sitahurumia, wala sitajuta; sawasawa na njia zako, na sawasawa na matendo yako, ndivyo watakavyokuhukumu, asema Bwana MUNGU. 15 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 16 Mwanadamu, tazama, ninakuondolea kwa pigo moja tunu, mteule wa macho yako; walakini hutaomboleza wala kulia, wala yasichuruzike machozi yako. 17 Ugua lakini si kwa sauti ya kusikiwa; usifanye matanga kwa ajili yake yeye aliyekufa; jipige kilemba chako, ukavae viatu vyako, wala usiifunike midomo yako, wala usile chakula cha watu. 18 Basi nalisema na watu asubuhi, na jioni mke wangu akafa; nami nalifanya asubuhi kama nilivyoagizwa. 19 Watu hao wakaniambia, Je! Hutaki kutuambia maana ya mambo haya kwetu, hata umefanya kama vile ufanyavyo. 20 Nikawaambia, Neno la Bwana lilinijia, kusema, 21 Uwaambie nyumba ya Israeli, Bwana MUNGU asema hivi; Angalieni, nitapatia unajisi patakatifu pangu, fahari ya uwezo wenu, mahali pa kutamaniwa na macho yenu, ambapo roho zenu zinapahurumia na wana wenu na binti zenu, mliowaacha nyuma, wataanguka kwa upanga. 22 Nanyi mtafanya kama mimi nilivyofanya; hamtaifunika midomo yenu, wala kula chakula cha watu. 23 Na vilemba vyenu vitakuwa juu ya vichwa vyenu, na viatu vyenu miguuni mwenu; hamtaomboleza wala kulia; lakini mtafifia katika maovu yenu, na kuugua kila mtu pamoja na mwenziwe. 24 Basi ndivyo Ezekielii atakavyokuwa ishara kwenu; ninyi mtatenda sawasawa na yote aliyoyatenda yeye; litakapokuja jambo hili, ndipo mtakapojua ya kuwa mimi ndimi Bwana MUNGU. 25 Nawe, mwanadamu, je! Haitakuwa hivi katika siku hiyo nitakapowaondolea nguvu zao, na furaha ya utukufu wao, na kilichotamaniwa na macho yao, ambacho walikiinulia mioyo yao, wana wao na binti zao, 26 kwamba katika siku iyo hiyo yeye atakayeokoka atakuja kwako, akusikize jambo hili kwa masikio yako? 27 Siku hiyo kinywa chako kitafumbuliwa kwake aliyeokoka, nawe utasema; hutakuwa bubu tena; ndivyo utakavyokuwa ishara kwao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 25

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, uwaelekezee wana wa Amoni uso wako, ukatabiri juu yao. 3 Uwaambie hao wana wa Amoni, Lisikieni neno la Bwana MUNGU; Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu umesema, Aha! Juu ya patakatifu pangu, palipotiwa unajisi; na juu ya nchi ya Israeli, ilipoharibiwa; na juu ya nyumba ya Israeli, walipokwenda kifungoni; 4 basi, kwa sababu hiyo, nitakutia katika mikono ya wana wa mashariki uwe milki yao, nao wataweka marago yao ndani yako, kufanya maskani zao ndani yako; watakula matunda yako, na kunywa maziwa yako. 5 Nami nitafanya Raba kuwa banda la ngamia, na wana wa Amoni kuwa mahali pa kulaza makundi; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 6 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu umepiga makofi, na kupiga mshindo kwa miguu yako, na kufurahi juu ya nchi ya Israeli, jeuri yote ya roho yako; 7 basi, tazama, nimenyosha mkono wangu juu yako, nami nitakutoa uwe mateka ya mataifa; nami nitakukatilia mbali na kabila za watu, nami nitakuangamiza, usiwe katika nchi hizo; nitakukomesha; nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 8 Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu Moabu na Seiri husema, Tazama, nyumba ya Israeli ni sawasawa na mataifa yote; 9 basi, tazama, nitawafunulia wana wa mashariki ubavu wa Moabu toka miji yake, toka miji yake iliyo mipakani mwake, utukufu wa nchi hiyo, Beth-yeshimothi, na Baal-meoni, na Kiriathaimu, 10 pamoja na wana wa Amoni, nami nitawatoa kuwa milki, ili wana wa Amoni wasikumbukwe kati ya mataifa, 11 nami nitatoa hukumu juu ya Moabu; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 12 Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa Edomu wametenda kinyume cha nyumba ya Yuda, kwa kujilipiza kisasi, nao wamekosa sana, na kujilipiza kisasi juu yao; 13 kwa sababu hiyo, Bwana MUNGU asema hivi; Nitanyosha mkono wangu juu ya Edomu, nitakatilia mbali nayo wanadamu na wanyama; nami nitaifanya kuwa ukiwa toka Temani; na mpaka Dedani wataanguka kwa upanga. 14 Nami nitaweka kisasi changu juu ya Edomu, kwa mkono wa watu wangu Israeli; nao watatenda mambo katika Edomu, kwa kadiri ya hasira yangu, na ghadhabu yangu, nao watakijua kisasi changu, asema Bwana MUNGU. 15 Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa Wafilisti wametenda mambo kwa kujilipiza kisasi, nao wamejilipiza kisasi kwa jeuri ya roho, ili kupaangamiza kwa uadui wa daima; 16 kwa sababu hiyo, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitanyosha mkono wangu juu ya Wafilisti, nami nitawakatilia mbali Wakerethi, na kuwaharibu wabakio pande za pwani. 17 Nami nitajilipiza kisasi kikuu, nikiwakemea kwa ukali; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapojilipiza kisasi juu yao.

Ezekieli 26

1 Ikawa katika mwaka wa kumi na mmoja, siku ya kwanza ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, Kwa sababu Tiro amesema juu ya Yerusalemu, Aha! Yeye amevunjika aliyekuwa lango la kabila za watu; amenigeukia; nitajazwa kwa kuwa sasa ameharibika; 3 basi Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ee Tiro, nami nitaleta mataifa mengi kupigana nawe, kama bahari iinuavyo mawimbi yake. 4 Nao wataziharibu kuta za Tiro, na kuibomoa minara yake; tena nitakwangua hata mavumbi yake yamtoke, na kumfanya kuwa jabali tupu. 5 Naye atakuwa mahali pa kutandazia nyavu za wavuvi kati ya bahari; maana mimi nimenena neno hili, asema Bwana MUNGU; naye atakuwa mateka ya mataifa. 6 Na binti zake walio katika mashamba watauawa kwa upanga; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 7 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitamleta Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mfalme wa wafalme, juu ya Tiro toka kaskazini, pamoja na farasi, na magari ya vita, na wapanda farasi, na jeshi, na watu wengi. 8 Atawaua binti zako kwa upanga katika mashamba; naye atafanya ngome juu yako, na kufanya maboma juu yako, na kuiinua ngao juu yako. 9 Naye ataweka vyombo vyake vya kubomolea mbele za kuta zako, na kwa mashoka yake ataiangusha chini minara yako. 10 Kwa sababu wingi wa farasi zake, mavumbi yao yatakufunika; kuta zako zitatetemeka kwa sababu ya mshindo wa wapanda farasi, na wa magurudumu, na wa magari ya vita, atakapoingia katika malango yako, kama watu waingiavyo katika mji uliobomolewa mahali. 11 Kwa kwato za farasi zake atazikanyaga njia zako zote; atawaua watu wako kwa upanga, na minara ya nguvu zako itashuka hata nchi. 12 Nao wataufanya utajiri wako kuwa mateka, na bidhaa yako kuwa mawindo; nao watazibomoa kuta zako, na kuziharibu nyumba zako zipendezazo; nao wataweka mawe yako, na miti yako, na mavumbi yako, kati ya maji. 13 Nami nitaikomesha sauti ya nyimbo zako, wala sauti ya vinubi vyako haitasikiwa tena. 14 Nami nitakufanya kuwa jabali tupu; utakuwa mahali pa kutandazia nyavu za wavuvi; hutajengwa tena; maana mimi, Bwana, nimenena neno hili, asema Bwana MUNGU. 15 Bwana MUNGU amwambia Tiro neno hili; Je! Visiwa havitatikisika kwa mshindo wa kuanguka kwako, watakapougua waliojeruhiwa, yatakapofanyika machinjo kati yako. 16 Ndipo wakuu wote wa bahari watashuka kutoka viti vyao vya enzi, na kuweka upande mavazi yao, na kuvua nguo zao zilizotiwa taraza; watajivika matetemeko; wataketi na kutetemeka kila dakika, na kukustaajabia, 17 Nao watakufanyia maombolezo, na kukuambia, Imekuwaje wewe kuharibika, wewe uliyekaliwa na wana-maji, mji wenye sifa, uliyekuwa na nguvu katika bahari, mji huo, na hao waliokaa ndani yake, waliowatia hofu wote waliokaa ndani yake! 18 Sasa visiwa vitatetemeka katika siku ya kuanguka kwako; naam, visiwa vilivyo katika bahari vitafadhaika, kwa sababu ya kuondoka kwako. 19 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Nitakapokufanya kuwa mji wa ukiwa, kama miji isiyokaliwa na watu; nitakapoleta vilindi vya bahari juu yako, na maji makuu yatakapokufunika; 20 ndipo nitakapokushusha pamoja nao washukao shimoni, uende kwa watu wa kale; nami nitakukalisha pande za chini za nchi; mahali palipokuwa ukiwa tangu zamani, pamoja nao washukao shimoni; ili usikaliwe na watu, wala usiweke utukufu wako katika nchi yao walio hai. 21 Nitakufanya kuwa kitu cha kutisha, wala hutakuwako tena; ujapotafutwa, lakini hutaonekana tena kabisa, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 27

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Na wewe, mwanadamu, mfanyie Tiro maombolezo; 3 umwambie Tiro, Ewe ukaaye penye maingilio ya bahari, uliye mchuuzi wa watu wa kabila nyingi, mpaka visiwa vingi, Bwana MUNGU asema hivi; Wewe, Tiro, umesema, Mimi ni ukamilifu wa uzuri. 4 Mipaka yako i kati ya moyo wa bahari; wajenzi wako wameukamilisha uzuri wako. 5 Mbao zako zote wamezifanya kwa misunobari itokayo Seniri; wametwaa mierezi ya Lebanoni ili kukufanyia mlingoti; 6 kwa mialoni ya Bashani wamefanya makasia yako; na sitaha zako wamezifanya kwa pembe iliyotiwa kazi ya njumu katika mti wa mihugu itokayo Kitimu. 7 Tanga lako lilikuwa la kitani safi itokayo Misri, iliyotiwa taraza, ili iwe bendera kwako; na chandalua chako kilikuwa cha rangi ya samawi na urujuani toka visiwa vya Elisha. 8 Wakaao Sidoni na Arvadi ndio waliovuta makasia yako; wana wako wenye akili, Ee Tiro, walikuwa ndani yako, ndio waliokuwa rubani zako. 9 Wazee wa Gebali na wenye akili wake walikuwa ndani yako, wenye kutia kalafati; merikebu zote za bahari na mabaharia wao walikuwa ndani yako, ili kubadiliana biashara yako. 10 Watu wa Uajemi na Ludi na Putu walikuwa katika jeshi lako, watu wako wa vita; walitungika ngao na chapeo ndani yako; wakadhihirisha uzuri wako. 11 Watu wa Arvadi, pamoja na jeshi lako, walikuwa juu ya kuta zako pande zote, na Wagamadi walikuwa ndani ya minara yako; walitungika ngao zao juu ya kuta zako pande zote; wakaukamilisha uzuri wako. 12 Tarshishi alikuwa mfanya biashara kwako, kwa sababu ya wingi wa utajiri wa kila aina; kwa fedha, na chuma, na bati, na risasi, walifanya biashara, wapate vitu vyako vilivyouzwa. 13 Uyunani na Tubali na Mesheki ndio waliokuwa wachuuzi wako; walitoa wanadamu, na vyombo vya shaba, kwa biashara yako. 14 Watu wa nyumba ya Togarma walifanya biashara, kwa farasi, naam, farasi za vita, na nyumbu, wapate vitu vyako vilivyouzwa. 15 Wadedani walikuwa wachuuzi wako, visiwa vingi vilikuwa soko la mkono wako; walikuletea pembe, na mpingo, ili kuvibadili. 16 Shamu alikuwa mfanya biashara kwako, kwa sababu ya wingi wa kazi za mkono wako walifanya biashara kwa zumaridi, na urujuani, na kazi ya taraza, na kitani safi, na marijani, na akiki, wapate vitu vyako vilivyouzwa. 17 Yuda, na nchi ya Israeli, walikuwa wachuuzi wako; walitoa badala ya bidhaa yako ngano ya Minithi, na mtama, na asali, na mafuta, na zeri. 18 Dameski alikuwa mfanya biashara kwako, kwa habari ya wingi wa kazi za mkono wako, kwa ajili ya wingi wa aina zote za utajiri; akaleta divai ya Helboni, na sufu nyeupe. 19 Wedani, na Yavani, walifanya biashara toka Uzali kwa vitu vyako; chuma kilichofuliwa, na mdalasini, na mchai, vilikuwa katika bidhaa yako. 20 Dedani alikuwa mchuuzi wako, kwa nguo za thamani za kutandikia farasi. 21 Arabuni, na wakuu wote wa Kedari, ndio waliokuwa wafanya biashara wa mkono wako; kwa wana-kondoo, na kondoo waume, na mbuzi; kwa hao walifanya biashara nawe. 22 Wachuuzi wa Sheba, na Raama, ndio waliokuwa wachuuzi wako; badala ya vitu vyako walitoa manukato yaliyo mazuri, na kila aina ya vito vya thamani, na dhahabu. 23 Harani, na Kane, na Adini, wachuuzi wa Sheba, na Ashuru, na Kilmadi, walikuwa wachuuzi wako. 24 Hao ndio waliokuwa wachuuzi wako, kwa vitu vya tunu, kwa vitumba vya nguo za samawi na kazi ya taraza, na masanduku ya mavazi ya thamani, yaliyofungwa kwa kamba, na kufanyizwa kwa mti wa mierezi, katika bidhaa yako. 25 Merikebu za Tarshishi zilikuwa misafara yako, kwa bidhaa yako; nawe ulijazwa sana, ukawa mtukufu sana, katika moyo wa bahari. 26 Wavuta makasia wako walikuleta katika maji makuu; upepo wa mashariki umekuvunja moyoni mwa bahari. 27 Mali zako, na bidhaa yako, na utajiri wako, wana-maji wako, na rubani zako, na wenye kutia kalafati wako, na wafanya biashara wako, na watu wako wa vita wote, walio ndani yako, pamoja na jeshi lako lote lililo ndani yako, wataanguka katika moyo wa bahari katika siku ya kuangamia kwako. 28 Kwa sauti ya vilio vya rubani zako viunga vyako vitatetema. 29 Na wote wavutao kasia, wana-maji, na rubani zote wa baharini, watashuka katika merikebu zao, na kusimama katika nchi kavu; 30 nao watasikizisha watu sauti zao juu yako, nao watalia kwa uchungu, na kutupa mavumbi juu ya vichwa vyao, na kugaagaa katika majivu; 31 nao watajifanya kuwa na upaa kwa ajili yako, na kujifunga nguo za magunia viunoni, nao watakulilia kwa uchungu wa roho, kwa maombolezo ya uchungu. 32 Na katika kulia kwao watakufanyia maombolezo, na kukuombolezea, wakisema, Ni nani aliye kama Tiro, kama yeye aliyenyamazishwa kati ya bahari? 33 Bidhaa zako zilipotoka katika bahari, uliwajaza watu wa kabila nyingi; uliwatajirisha wafalme wa dunia, kwa wingi wa mali zako, na kwa utajiri wako. 34 Wakati ulipovunjwa na bahari, katika vilindi vya maji, bidhaa zako na jeshi lako lote walianguka kati yako. 35 Wote wakaao katika visiwa vile watakustaajabia, na wafalme wao wameogopa sana, wamefadhaika nyuso zao. 36 Wafanya biashara kati ya kabila za watu wakuzomea; umekuwa kitu cha kutisha, wala hutakuwapo tena milele.

Ezekieli 28

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Mwanadamu, mwambie mkuu wa Tiro, Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa moyo wako umeinuka, nawe umesema, Mimi ni Mungu, nami nimeketi katika kiti cha Mungu, kati ya bahari; lakini u mwanadamu wala si Mungu, ujapokuwa umeweka moyo wako kama moyo wa Mungu. 3 Tazama, una hekima kuliko Danieli; hapana neno la siri watu wawezalo kukuficha; 4 kwa hekima yako na kwa fahamu zako umejipatia utajiri, nawe umepata dhahabu na fedha katika hazina zako; 5 kwa hekima yako nyingi, na kwa biashara yako, umeongeza utajiri wako, na moyo wako umeinuka kwa sababu ya utajiri wako; 6 basi, kwa hiyo, Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa umeweka moyo wako kama moyo wa Mungu; 7 basi, tazama, nitaleta wageni juu yako, watu wa mataifa wenye kutisha; nao watafuta panga zao juu ya uzuri wa hekima yako, nao watautia uchafu mwangaza wako. 8 Watakushusha hata shimoni; nawe utakufa kifo chao waliouawa kati ya bahari. 9 Je! Utazidi kusema mbele yake huyo akuuaye, Mimi ni Mungu? Lakini u mwanadamu, wala si Mungu, mkononi mwake akutiaye jeraha. 10 Utakufa kifo cha hao wasiotahiriwa, kwa mikono ya wageni; kwa maana mimi nimenena neno hili, asema Bwana MUNGU. 11 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 12 Mwanadamu, umfanyie maombolezo mfalme wa Tiro, umwambie, Bwana MUNGU asema hivi; Wewe wakitia muhuri kipimo, umejaa hekima, na ukamilifu wa uzuri. 13 Ulikuwa ndani ya Adeni, bustani ya Mungu; kila jiwe la thamani lilikuwa kifuniko chako, akiki, na yakuti manjano, na almasi, na zabarajadi, na shohamu, na yaspi, na yakuti samawi, na zumaridi, na baharamani, na dhahabu; kazi ya matari yako na filimbi zako ilikuwa ndani yako; katika siku ya kuumbwa kwako zilitengenezwa tayari. 14 Wewe ulikuwa kerubi mwenye kutiwa mafuta afunikaye; nami nalikuweka hata ukawa juu ya mlima mtakatifu wa Mungu, umetembea huko na huko kati ya mawe ya moto. 15 Ulikuwa mkamilifu katika njia zako tangu siku ile ulipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yako. 16 Kwa wingi wa uchuuzi wako watu walikujaza udhalimu ndani yako, nawe umetenda dhambi; kwa sababu hiyo nimekutoa kwa nguvu katika mlima wa Mungu, kama kitu kilicho najisi; nami nimekuangamiza, Ewe kerubi ufunikaye, utoke katika mawe hayo ya moto. 17 Moyo wako uliinuka kwa sababu ya uzuri wako; umeiharibu hekima yako kwa sababu ya mwangaza wako; nimekutupa chini, nimekulaza mbele ya wafalme, wapate kukutazama. 18 Kwa wingi wa maovu yako, katika uovu wa uchuuzi wako, umepatia unajisi patakatifu pako; basi nimetokeza moto kutoka ndani yako, nao umekuteketeza, nami nimekufanya kuwa majivu juu ya nchi, machoni pa watu wote wakutazamao. 19 Wote wakujuao kati ya kabila za watu watakustaajabia; umekuwa kitu cha kutisha, wala hutakuwapo tena hata milele. 20 Neno la Bwana likanijia, kusema, 21 Mwanadamu, uuelekezee Sidoni uso wako, ukatabiri juu yake, 22 useme, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ee Sidoni, nami natukuzwa kati yako; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapokuwa nimetekeleza hukumu zangu ndani yake, na kutakasika ndani yake. 23 Maana nitampelekea tauni, na damu, katika njia kuu zake, na hao waliotiwa jeraha wataanguka kati yake, kwa upanga juu yake pande zote; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 24 Wala hautakuwapo mchongoma uchomao kwa nyumba ya Israeli; wala mwiba uumizao miongoni mwa wote wamzungukao, waliowatenda mambo ya jeuri; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana MUNGU. 25 Bwana MUNGU asema hivi; Nitakapokuwa nimewakusanya nyumba ya Israeli, na kuwatoa katika watu ambao wametawanyika kati yao, na kutakasika kati yao machoni pa mataifa, ndipo watakapokaa katika nchi yao wenyewe, niliyompa mtumishi wangu, Yakobo. 26 Nao watakaa humo salama; naam, watajenga nyumba, na kupanda mashamba ya mizabibu, na kukaa salama; nitakapokuwa nimetekeleza hukumu zangu juu ya watu wote, wanaowatenda mambo ya jeuri pande zote; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wao.

Ezekieli 29

1 Katika mwaka wa kumi, mwezi wa kumi, siku ya kumi na mbili ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, elekeza uso wako juu ya Farao, mfalme wa Misri, ukatabiri juu yake, na juu ya Misri yote; 3 nena, useme, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ewe Farao, mfalme wa Misri, joka kubwa aoteaye kati ya mito yake, aliyesema, Mto wangu ni wangu mwenyewe, nami nimeufanya kwa ajili ya nafsi yangu. 4 Nami nitatia kulabu katika taya zako, nami nitawashikamanisha samaki wa mito yako na magamba yako; nami nitakutoa katika mito yako, pamoja na samaki wa mito yako walioshikamana na magamba yako. 5 Nami nitakuacha hali umetupwa jangwani, wewe na samaki wote wa mito yako; utaanguka juu ya uso wa uwanda; hutakusanywa, wala kuwekwa pamoja; nimekutoa uwe chakula cha wanyama wa nchi, na cha ndege wa angani. 6 Na watu wote wakaao Misri watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, kwa sababu wamekuwa mwanzi wa kutegemewa kwa nyumba ya Israeli. 7 Walipokushika kwa mkono wako, ulivunjika, ukawararua mabega yao yote; nao walipokutegemea, ulivunjika, ukawatetemesha viuno vyao vyote. 8 Basi, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitaleta upanga juu yako, nami nitakatilia mbali nawe wanadamu na wanyama. 9 Nayo nchi ya Misri itakuwa ukiwa na jangwa; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana; kwa sababu amesema, Mto huu ni wangu, nami nimeufanya. 10 Basi, tazama, mimi ni juu yako, na juu ya mito yako, nami nitaifanya nchi ya Misri kuwa jangwa tupu, na ukiwa, toka Migdoli hata Sewene, hata mpaka wa Kushi. 11 Hautapita kati yake mguu wa mwanadamu, wala hautapita kati yake mguu wa mnyama, wala haitakaliwa na watu, muda wa miaka arobaini. 12 Nami nitaifanya nchi ya Misri kuwa ukiwa, kati ya nchi zilizo ukiwa, na miji yake, kati ya miji iliyoharibika, itakuwa maganjo muda wa miaka arobaini; nami nitawatawanya Wamisri kati ya mataifa, nami nitawatapanya kati ya nchi mbalimbali. 13 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Mwisho wa miaka arobaini nitawakusanya Wamisri, na kuwatoa katika hizo kabila za watu, ambazo walitawanyika kati yao; 14 nami nitawarejeza Wamisri walio katika hali ya kufungwa, nami nitawarudisha hata nchi ya Pathrosi, hata nchi ya kuzaliwa kwao; na huko watakuwa ufalme duni. 15 Utakuwa duni kuliko falme zote; wala hautajiinua tena juu ya mataifa; nami nitawapunguza, ili wasitawale tena juu ya mataifa. 16 Wala hautakuwa tena tumaini la nyumba ya Israeli, kufanya maovu yakumbukwe, watakapogeuka kuangalia nyuma yao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana MUNGU. 17 Ikawa katika mwaka wa ishirini na saba, mwezi wa kwanza, siku ya kwanza ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 18 Mwanadamu, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alilihudumisha jeshi lake huduma kuu juu ya Tiro; kila kichwa kilitiwa upaa, na kila bega liliambuliwa ngozi, lakini alikuwa hana mshahara uliotoka Tiro, wala yeye wala jeshi lake, kwa huduma ile aliyohudumu juu yake. 19 Basi, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitampa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, hiyo nchi ya Misri; naye atawachukua watu wake jamii yote pia, na kutwaa mateka yake, na kutwaa mawindo yake, nayo yatakuwa ndio mshahara wa jeshi lake. 20 Nimempa nchi ya Misri kuwa malipo ya huduma aliyohudumu, kwa sababu walifanya kazi kwa ajili yangu; asema Bwana MUNGU. 21 Siku ile nitawachipushia nyumba ya Israeli pembe, nami nitakujalia kufumbua kinywa kati yao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 30

1 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 2 Mwanadamu, tabiri, useme, Bwana MUNGU asema hivi; Pigeni makelele ya uchungu, Ole wa siku ile! 3 Kwa maana siku ile i karibu, siku ile ya Bwana i karibu, siku ya mawingu; itakuwa wakati wa mataifa. 4 Na upanga utakuja juu ya Misri, na dhiki itakuwa katika Kushi, watakapoanguka watu waliouawa katika Misri, nao watauondoa wingi wa watu wake, na misingi yake itabomolewa. 5 Kushi, na Putu, na Ludi, na watu wote waliochanganyika, na Kubu, na wana wa nchi ya agano, wataanguka kwa upanga pamoja nao. 6 Bwana asema hivi; Nao pia wanaoitegemeza Misri wataanguka, na kiburi cha uwezo wake kitashuka; toka Migdoli hata Sewene, wataanguka ndani yake kwa upanga, asema Bwana MUNGU. 7 Nao watakuwa ukiwa, kati ya nchi zilizo ukiwa, na miji yake itakuwamo kati ya miji iliyoharibika. 8 Nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoweka moto katika Misri, na hao wote wamsaidiao watakapoangamia. 9 Katika siku hiyo watatoka wajumbe mbele zangu katika merikebu, ili kuwatia hofu Wakushi, wanaojiona kuwa salama, na dhiki itakuwa juu yao, vile vile kama katika siku ya Misri; kwa maana, tazama, inakuja. 10 Bwana MUNGU asema hivi; Pia nitaukomesha wingi wa watu wa Misri, kwa mkono wa Nebukadreza, mfalme wa Babeli. 11 Yeye, na watu wake pamoja naye, watu wa mataifa watishao, wataletwa waingie katika nchi waiharibu, nao watafuta panga zao wapigane na Misri, na kuijaza nchi wale waliouawa. 12 Nami nitaikausha mito, na kuiuza nchi, na kuitia katika mikono ya watu wabaya; nami nitaifanya nchi kuwa ukiwa, na watu wote walio ndani yake, kwa mkono wa wageni; mimi, Bwana, nimenena neno hili. 13 Bwana MUNGU asema hivi; Pia nitaviharibu vinyago, nami nitavikomesha vitu vya ubatili katika Nofu, wala hapatakuwa na mkuu tena atokaye katika nchi ya Misri, nami nitatia hofu katika nchi ya Misri. 14 Nami nitaifanya Pathrosi kuwa ukiwa, nami nitatia moto katika Soani, nami nitatekeleza hukumu katika No. 15 Nami nitamwaga ghadhabu yangu juu ya Sini, ngome ya Misri, nami nitakatilia mbali wingi wa watu wa No. 16 Nami nitatia moto katika Misri; Sini itakuwa katika dhiki kuu, na No itavunjika kabisa; na Nofu itakuwa na adui wakati wa mchana. 17 Vijana wa Oni, na wa Pi-besethi, wataanguka kwa upanga; na miji hiyo itakwenda utumwani. 18 Huko Tapanesi nako mchana utakuwa giza, nitakapovunja huko kongwa za Misri, na kiburi cha uwezo wake kitakoma ndani yake, na katika habari zake, wingu litaifunika, na binti zake watakwenda utumwani. 19 Hivyo ndivyo nitakavyotekeleza hukumu katika Misri; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 20 Ikawa katika mwaka wa kumi na mmoja, mwezi wa kwanza, siku ya saba ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 21 Mwanadamu, nimeuvunja mkono wa Farao, mfalme wa Misri, na tazama, haukufungwa ili kuutia dawa, haukuzongwa kwa kitambaa, upate kuwa na nguvu za kushika upanga. 22 Basi Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu ya Farao, mfalme wa Misri, nami nitamvunja mikono yake, mkono ulio wenye nguvu, na huo uliovunjika, nami nitauangusha upanga ulio katika mkono wake. 23 Nami nitawatawanya Wamisri kati ya mataifa, na kuwatapanya kati ya nchi mbalimbali. 24 Nami nitaitia nguvu mikono ya mfalme wa Babeli, na kuutia upanga wangu katika mkono wake, bali mikono ya Farao nitaivunja, naye ataugua mbele yake, kwa mauguzi ya mtu aliyetiwa jeraha ya kumfisha. 25 Nami nitaitegemeza mikono ya mfalme wa Babeli, na mikono ya Farao itaanguka; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoutia upanga wangu katika mkono wa mfalme wa Babeli, naye ataunyosha juu ya nchi ya Misri. 26 Nami nitawatawanya Wamisri kati ya mataifa, na kuwatapanya kati ya nchi mbalimbali; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 31

1 Ikawa katika mwaka wa kumi na mmoja, mwezi wa tatu, siku ya kwanza ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, mwambie Farao mfalme wa Misri, na jamii ya watu wake, Je! Umefanana na nani katika ukuu wako? 3 Tazama, Mwashuri alikuwa mwerezi katika Lebanoni, wenye matawi mazuri, na kifuniko chenye uvuli, na kimo kirefu; na kilele chake kilikuwa kati ya matawi mapana. 4 Maji yalimlisha, vilindi vilimsitawisha; mito yake ilipita pande zote za miche yake; naye akapeleka mifereji yake kwa miti yote ya kondeni. 5 Basi kimo chake kilitukuzwa kuliko miti yote ya kondeni, na vitanzu vyake viliongezeka; matawi yake yakawa marefu, kwa sababu ya maji mengi, alipoyachipuza. 6 Ndege wote wa angani walifanya vioto vyao katika vitanzu vyake, na chini ya matawi yake wanyama wote wa kondeni walizaa watoto wao, na chini ya uvuli wake mataifa makuu yote walikaa. 7 Basi hivyo alikuwa mzuri katika ukuu wake, katika urefu wa matawi yake; maana mizizi yake ilikuwa karibu na maji mengi. 8 Mierezi ya bustani ya Mungu haikuweza kumficha; misunobari haikuwa kama vitanzu vyake, na miamori haikuwa kama matawi yake, wala bustanini mwa Mungu hamkuwa na mti wo wote uliofanana naye kwa uzuri. 9 Nalimfanya kuwa mzuri kwa wingi wa matawi yake; hata miti yote ya Adeni, iliyokuwa ndani ya bustani ya Mungu, ilimwonea wivu. 10 Basi Bwana MUNGU asema hivi; kwa kuwa umetukuzwa kimo chako, naye ameweka kilele chake kati ya mawingu, na moyo wake umeinuka kwa urefu wake; 11 mimi nitamtia katika mikono yake aliye mkuu kati ya mataifa; naye atamtenda mambo; nimemfukuza kwa sababu ya uovu wake. 12 Na wageni, watu wa mataifa watishao, wamemkatilia mbali na kumwacha; juu ya milima na katika mabonde yote matawi yake yameanguka, na vitanzu vyake vimevunjika karibu na mifereji yote ya nchi; na watu wote wa dunia wameshuka, wakitoka katika uvuli wake na kumwacha. 13 Juu ya magofu yake ndege wote wa angani watakaa, na wanyama wote wa jangwani watakuwa juu ya matawi yake; 14 kusudi mti wo wote, ulio karibu na maji, usijitukuze kwa sababu ya kimo chake, wala usitie kilele chake kati ya mawingu, wala mashujaa wake wasisimame katika kimo chao kirefu, naam, wote wanywao maji; maana wote wametolewa wafe, waende pande za chini za nchi, kati ya wanadamu, pamoja nao washukao shimoni. 15 Bwana MUNGU asema hivi, Katika siku ile alipotelemka mpaka kuzimu naliamuru matanga, nalikifunika kilindi kwa ajili yake, nikiizuia mito yake, nayo maji makuu yalizuiwa; naliamuru Lebanoni kumwombolezea, na miti yote ya kondeni ilizimia kwa ajili yake. 16 Niliwatetemesha mataifa kwa mshindo wa kuanguka kwake, hapo nilipomtupa chini mpaka kuzimu, pamoja nao washukao shimoni; na miti yote ya Adeni, miti iliyo miteule na iliyo mizuri ya Lebanoni, yote inywayo maji, ilifarijika pande za chini za nchi. 17 Hao nao walitelemka kuzimuni pamoja naye kwa watu waliouawa kwa upanga; naam, wale waliokuwa mkono wake, waliokaa chini ya uvuli wake kati ya mataifa. 18 Umefanana na nani, hivi katika utukufu na ukuu, kati ya miti ya Adeni? Lakini utashushwa pamoja na miti ya Adeni, hata pande za chini za nchi; utalala kati ya hao wasiotahiriwa; pamoja na hao waliouawa kwa upanga. Huyu ndiye Farao, na jamii yote ya watu wake, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 32

1 Ikawa katika mwaka wa kumi na mbili, mwezi wa kumi na mbili, siku ya kwanza ya mwezi, neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, mfanyie Farao, mfalme wa Misri, maombolezo, umwambie, Ulifananishwa na mwana-simba wa mataifa; lakini umekuwa kama joka katika bahari; nawe watoka kwa nguvu pamoja na mito yako, na kuyachafua maji kwa miguu yako, na kuitia uchafu mito yao. 3 Bwana MUNGU asema hivi; Nitautanda wavu wangu juu yako, kwa kusanyiko la watu wa kabila nyingi; nao watakuvua katika jarife langu. 4 Nami nitakuacha juu ya nchi kavu, nitakutupa juu ya uso wa uwanda, nami nitawaleta ndege wote wa angani watue juu yako, nami nitawashibisha wanyama wa dunia yote kwako wewe. 5 Nami nitaweka nyama yako juu ya milima, na kuyajaza mabonde kwa urefu wako. 6 Tena kwa damu yako nitainywesha nchi, ambayo waogelea juu yake, hata milimani; na mifereji ya maji itajawa nawe. 7 Nami nitakapokuzimisha, nitazifunikiza mbingu, na kuzifanya nyota zake kuwa giza; nami nitalifunika jua kwa wingu, wala mwezi hautatoa nuru yake. 8 Mianga yote ya mbinguni iangazayo nitaifanya kuwa giza juu yako, nami nitatia giza katika nchi yako, asema Bwana MUNGU. 9 Tena nitawakasirisha watu wengi mioyo yao, nitakapoleta uangamivu wako kati ya mataifa, uingie katika nchi ambazo hukuzijua. 10 Nami nitawashangaza watu wa kabila nyingi kwa habari zako, na wafalme wao wataogopa sana kwa ajili yako, nitakapoutikisa upanga wangu mbele yao; nao watatetemeka kila dakika, kila mtu kwa ajili ya uhai wake, katika siku ya kuanguka kwako. 11 Maana Bwana MUNGU asema hivi; Upanga wa mfalme wa Babeli utakujilia. 12 Kwa panga za mashujaa nitawaangusha watu wako wote jamii; hao wote ni watu wa mataifa watishao, nao watakiharibu kiburi cha Misri, na jamii ya watu wake wengi wataangamia. 13 Tena nitawaharibu wanyama wake wote, toka kando ya maji mengi; na mguu wa mwanadamu hautayatibua tena, wala kwato za mnyama hazitayatibua. 14 Ndipo nitakapoyafanya maji yao kuwa safi, na kuiendesha mito yao kama mafuta, asema Bwana MUNGU. 15 Nitakapoifanya nchi ya Misri kuwa ukiwa na jangwa, nchi iliyopungukiwa na vitu vilivyoijaza, nitakapowapiga watu wote wakaao ndani yake, ndipo watakapojua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 16 Hayo ndiyo maombolezo watakayoomboleza; binti za mataifa wataomboleza kwa hayo; kwa hayo wataomboleza kwa ajili ya Misri, na kwa ajili ya watu wake wote jamii, asema Bwana MUNGU. 17 Ikawa katika mwaka wa kumi na mbili, siku ya kumi na tano ya mwezi, neno la Bwana likanijia kusema, 18 Mwanadamu, walilie watu wa Misri. Wote jamii ukawabwage, naam, yeye, na binti za mataifa mashuhuri, hata pande za chini za nchi, pamoja na watu washukao shimoni. 19 Umemshinda nani kwa uzuri? Shuka, ukalazwe pamoja na wasiotahiriwa. 20 Wataanguka kati ya watu waliouawa kwa upanga; ametokwa apigwe na upanga; mvuteni aende mbali pamoja na watu wake wote jamii. 21 Walio hodari watasema naye, toka kati ya kuzimu pamoja nao wamsaidiao; wameshuka wamelala kimya, hata wasiotahiriwa, hali wameuawa kwa upanga. 22 Ashuru yuko huko, na watu wake wote jamii; makaburi yake yamzunguka; wote pia wameuawa, wameanguka kwa upanga, 23 ambao makaburi yao yamewekwa pande za shimo zilizo mbali sana, wote jamii wamezunguka kaburi lake; wote pia wameuawa, wameanguka kwa upanga, waliofanya utisho katika nchi yao walio hai. 24 Elamu yuko huko, na watu wake wote jamii, pande zote za kaburi lake; wote pia wameuawa, wameanguka kwa upanga, walioshuka hali hawana tohara hata pande za chini ya nchi; ambao waliwatia watu hofu katika nchi ya walio hai, nao wamechukua aibu yao, pamoja nao washukao shimoni. 25 Wamemwekea kitanda kati ya hao waliouawa, pamoja na watu wake wote jamii; makaburi yake yamzunguka; wote pia hawakutahiriwa, wameuawa kwa upanga; maana maogofyo yao yalifanyika katika nchi ya walio hai, nao wamechukua aibu yao, pamoja nao washukao shimoni; amewekwa kati ya hao waliouawa. 26 Mesheki yuko huko, na Tubali, na watu wake wote jamii; makaburi yake yamzunguka; wote pia hawakutahiriwa, wameuawa kwa upanga; maana walifanya utisho wao katika nchi ya walio hai. 27 Je! Wasilale pamoja na mashujaa wao wasiotahiriwa, walioanguka, walioshuka kuzimu pamoja na silaha zao za vita, ambao wameweka panga zao chini ya vichwa vyao, na maovu yao mifupani mwao? Maana waliwatisha mashujaa katika nchi ya walio hai. 28 Lakini utavunjika kati ya hao wasiotahiriwa, nawe utalala pamoja nao waliouawa kwa upanga. 29 Edomu yuko huko, wafalme wake, na wakuu wake wote, ambao katika uwezo wao wamelazwa pamoja nao waliouawa kwa upanga; watalala pamoja na hao wasiotahiriwa, na pamoja na hao washukao shimoni. 30 Wakuu wa kaskazini wako huko, wote pia, na Wasidoni, wote walioshuka pamoja na hao waliouawa; kwa sababu ya utisho walioufanya katika uwezo wao wamefedheheka, nao wamelala hali hawana tohara, pamoja nao waliouawa kwa upanga, nao wanachukua aibu yao, pamoja nao washukao shimoni. 31 Farao atawaona, naye atapata faraja juu ya watu wake wote jamii; naam, Farao, jeshi lake lote waliouawa kwa upanga, asema Bwana MUNGU. 32 Kwa maana nimeweka utisho wake katika nchi ya walio hai; naye atalazwa kati yao wasiotahiriwa, pamoja na hao waliouawa kwa upanga; yeye Farao na watu wake wote jamii, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 33

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, sema na wana wa watu wako, uwaambie, Hapo nitakapoleta upanga juu ya nchi, watu wa nchi hiyo wakimtwaa mtu mmoja miongoni mwao, na kumweka awe mlinzi wao; 3 ikiwa, aonapo upanga unakuja juu ya nchi hiyo, apiga tarumbeta na kuwaonya watu; 4 basi mtu awaye yote aisikiaye sauti ya tarumbeta, wala haonywi, upanga ukija na kumwondoa, damu yake itakuwa juu ya kichwa chake mwenyewe. 5 Aliisikia sauti ya tarumbeta, wala hakuonywa; damu yake itakuwa juu yake; lakini kama angalionywa, angalijiokoa roho yake. 6 Bali mlinzi akiona upanga unakuja, kama hapigi tarumbeta, wala watu hawakuonywa, na upanga ukaja ukamwondoa mtu awaye yote miongoni mwao; ameondolewa huyo katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwa mlinzi huyo. 7 Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. 8 Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. 9 Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako. 10 Na wewe, mwanadamu, sema na nyumba ya Israeli; Ninyi mwasema hivi, kwamba, Makosa yetu na dhambi zetu ni juu yetu, nasi tumedhoofika katika dhambi hizo; basi tungewezaje kuwa hai? 11 Waambie, Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli? 12 Na wewe, mwanadamu, waambie wana wa watu wako, Haki yake mwenye haki haitamwokoa, katika siku ya kukosa kwake; na kwa habari ya uovu wake mtu mwovu, hataanguka kwa ajili ya uovu huo, siku ile atakapoghairi na kuuacha uovu wake; wala yeye aliye mwenye haki hataweza kuishi kwa haki yake, siku ile atakapotenda dhambi. 13 Nimwambiapo mwenye haki, ya kwamba hakika ataishi; kama akiitumainia haki yake, akatenda uovu, basi katika matendo yake ya haki, hata mojawapo halitakumbukwa; bali katika uovu wake alioutenda, atakufa katika uovu huo. 14 Tena, nimwambiapo mtu mwovu, Hakika utakufa; kama akighairi, na kuiacha dhambi yake, na kutenda yaliyo halali na haki; 15 kama mtu mwovu akirudisha rehani, na kumrudishia mtu mali yake aliyomnyang'anya, akizifuata sheria za uzima, asitende uovu wo wote; hakika ataishi, hatakufa. 16 Katika dhambi zake zote alizozitenda, hata mojawapo haitakumbukwa juu yake; ametenda yaliyo halali na haki; hakika ataishi. 17 Walakini wana wa watu wako husema, Njia ya Bwana si sawa; lakini watu hao, njia yao si sawa. 18 Mwenye haki ageukapo, na kuiacha haki yake, na kutenda maovu, atakufa katika maovu hayo. 19 Na mtu mbaya ageukapo, na kuuacha ubaya wake, na kutenda yaliyo halali na haki, ataishi kwa matendo hayo. 20 Lakini ninyi husema, Njia ya Bwana si sawa. Ee nyumba ya Israeli, nitawahukumu ninyi; kila mtu kwa kadiri ya njia zake. 21 Ikawa, katika mwaka wa kumi na mbili wa kuhamishwa kwetu, mwezi wa kumi, siku ya tano ya mwezi, mtu mmoja aliyekuwa ametoroka toka Yerusalemu akanijia, akisema, Mji umepigwa. 22 Basi mkono wa Bwana umekuwa juu yangu wakati wa jioni, kabla hajafika yeye aliyetoroka; naye alikuwa amenifumbua kinywa changu, hata aliponijia wakati wa asubuhi; na kinywa changu kilikuwa wazi, wala sikuwa bubu tena. 23 Neno la Bwana likanijia, kusema, 24 Mwanadamu, watu wale wakaao mahali palipoharibika katika nchi ya Israeli husema ya kwamba, Ibrahimu alikuwa mmoja, akairithi nchi hii; lakini sisi tu watu wengi; tumepewa nchi hii iwe urithi wetu. 25 Basi, waambie, Bwana MUNGU asema hivi; Mnakula nyama pamoja na damu yake, na kuviinulia vinyago vyenu macho yenu, na kumwaga damu; je, mtaimiliki nchi hii? 26 Mnategemea upanga wenu, mnatenda machukizo, mnanajisi kila mtu mke wa jirani yake; je! Mtaimiliki nchi hii? 27 Hivi ndivyo utakavyowaambia, Bwana MUNGU asema hivi; Kama mimi niishivyo, hakika watu wale wakaao mahali palipoharibika wataanguka kwa upanga, naye mtu aliye katika uwanda, nitamtoa na kuwapa wanyama wakali, ili aliwe; na hao walio ndani ya ngome na mapango watakufa kwa tauni. 28 Nami nitaifanya nchi kuwa ukiwa na ajabu, na kiburi cha uwezo wake kitakoma; nayo milima ya Israeli itakuwa ukiwa, asipite mtu. 29 Ndipo watakapojua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoifanya nchi kuwa ukiwa na ajabu, kwa sababu ya machukizo yao yote waliyoyatenda. 30 Nawe, mwanadamu, wana wa watu wako husimulia habari zako karibu na kuta, na ndani ya milango ya nyumba zao, na kuambiana, kila mtu na ndugu yake, wakisema, Haya! Twende tukasikie ni neno gani hilo litokalo kwa Bwana. 31 Nao huja kwako kama watu wajavyo, nao hukaa mbele yako kama watu wangu, nao husikia maneno yako, wasiyatende; maana kwa vinywa vyao hujifanya kuwa wenye upendo mwingi, lakini mioyo yao inatafuta faida yao. 32 Na tazama, wewe umekuwa kwao kama wimbo mzuri sana, wa mtu mwenye sauti ipendezayo, awezaye kupiga kinanda vizuri; maana, wasikia maneno yako, lakini hawayatendi. 33 Na hayo yatakapokuwapo (tazama, yanakuja), ndipo watakapojua ya kuwa nabii amekuwapo kati yao.

Ezekieli 34

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, toa unabii juu ya wachungaji wa Israeli, toa unabii, uwaambie, naam, hao wachungaji, Bwana MUNGU asema hivi; Ole wao wachungaji wa Israeli, wanaojilisha wenyewe; je! Haiwapasi wachungaji kuwalisha kondoo? 3 Mnawala walionona, mnajivika manyoya, mnawachinja walionona; lakini hamwalishi kondoo. 4 Wagonjwa hamkuwatia nguvu, wala hamkuwaponya wenye maradhi, wala hamkuwafunga waliovunjika, wala hamkuwarudisha waliofukuzwa, wala hamkuwatafuta waliopotea; bali kwa nguvu na kwa ukali mmewatawala. 5 Nao wakatawanyika, kwa sababu hapakuwa na mchungaji; wakawa chakula cha wanyama- mwitu, wakatawanyika. 6 Kondoo zangu walitanga-tanga katika milima yote, na juu ya kila kilima kirefu; naam, kondoo zangu walitawanyika juu ya uso wote wa dunia; wala hapakuwa na mtu aliyewaulizia, wala kuwatafuta. 7 Basi, enyi wachungaji, lisikieni neno la Bwana; 8 Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, kwa sababu kondoo zangu walikuwa mateka, kondoo zangu wakawa chakula cha wanyama-mwitu wote, kwa sababu hapakuwa na mchungaji, wala wachungaji wangu hawakutafuta kondoo zangu, bali wachungaji walijilisha wenyewe wala hawakuwalisha kondoo zangu; 9 kwa sababu hiyo, enyi wachungaji, lisikieni neno la Bwana; 10 Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu ya wachungaji; nami nitawataka kondoo zangu mikononi mwao, nami nitawaachisha hiyo kazi ya kuwalisha kondoo; nao wachungaji hawatajilisha wenyewe tena; nami nitawaokoa kondoo zangu vinywani mwao, wasiwe tena chakula chao. 11 Maana, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia. 12 Kama vile mchungaji atafutavyo kondoo zake, siku ile anapokuwa kati ya kondoo zake waliotawanyika; ndivyo nitakavyowatafuta kondoo zangu; nami nitawaokoa katika mahali pote walipotawanyika, katika siku ya mawingu na giza. 13 Nami nitawatoa katika watu wa mataifa, na kuwakusanya katika nchi zote, nami nitawarudisha katika nchi yao wenyewe; nami nitawalisha juu ya milima ya Israeli, kando ya mifereji ya maji; na katika mahali pote pa nchi panapokaliwa na watu. 14 Nami nitawalisha malisho mema, pa juu ya milima ya mahali palipoinuka pa Israeli litakuwa zizi lao; huko watalala katika zizi jema; nao watakula malisho mema, juu ya milima ya Israeli. 15 Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza, asema Bwana MUNGU. 16 Nami nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa; nao wanono na wenye nguvu nitawaharibu; nitawalisha hukumu. 17 Na kwa habari zenu, Enyi kundi langu, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nahukumu kati ya mnyama na mnyama, kondoo waume na mbuzi waume pia. 18 Je! Mwaona ya kuwa ni neno dogo ninyi kulishwa malisho mema, hata mkawa hamna budi hukanyaga kwa miguu yenu yaliyosalia? Na kuwa mmekunywa maji yaliyo safi, nanyi hamna budi kuyatibua kwa miguu yaliyobaki? 19 Na kwa habari za kondoo zangu, wao wanakula hayo mliyoyakanyaga kwa miguu yenu, nao wanakunywa maji mliyoyatibua kwa miguu yenu. 20 Kwa sababu hiyo, Bwana MUNGU awaambia hivi; Tazama, mimi, naam, mimi, nitahukumu kati ya wanyama walionona na wanyama waliokonda. 21 Kwa kuwa mmesukuma kwa ubavu, na kwa mabega, na kuwapiga wenye maradhi kwa pembe zenu, hata mkawatawanyia mbali; 22 basi mimi nitaliokoa kundi langu, wala hawatakuwa mateka tena; nami nitahukumu kati ya mnyama na mnyama. 23 Nami nitaweka mchungaji mmoja juu yao, naye atawalisha, naam, mtumishi wangu, Daudi; yeye atawalisha, naye atakuwa mchungaji wao. 24 Na mimi, Bwana, nitakuwa Mungu wao, na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mkuu kati yao; mimi, Bwana, nimesema haya. 25 Nami nitafanya agano la amani nao, nami nitawakomesha wanyama wakali kati yao; nao watakaa salama jangwani, na kulala misituni. 26 Nami nitawafanya wao, na mahali palipo pande zote za mlima wangu, kuwa baraka, nami nitaleta manyunyu kwa wakati wake; yatakuwako manyunyu ya baraka. 27 Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapovunja vifungo vya kongwa lao, na kuwaokoa katika mikono ya watu wale waliowatumikisha. 28 Hawatakuwa mateka ya makafiri tena, wala mnyama wa nchi hatawala; bali watakaa salama salimini, wala hapana mtu atakayewatia hofu. 29 Nami nitawainulia miche iwe sifa njema, wala hawataangamizwa kwa njaa katika nchi yao tena, wala hawatachukua tena aibu ya makafiri. 30 Nao watajua ya kuwa mimi, Bwana, Mungu wao, ni pamoja nao, na ya kuwa wao, nyumba ya Israeli, ni watu wangu, asema Bwana MUNGU. 31 Na ninyi, kondoo zangu, kondoo za malisho yangu, ni wanadamu, na mimi ni Mungu wenu, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 35

1 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, kaza uso wako juu ya mlima Seiri, ukatabiri juu yake, 3 uuambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ee mlima Seiri, nami nitaunyosha mkono wangu juu yako, nami nitakufanya kuwa ukiwa na ajabu. 4 Miji yako nitaiharibu, nawe utakuwa ukiwa; nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 5 Kwa kuwa umekuwa na uadui usiokoma, nawe umewatoa wana wa Israeli wapigwe kwa nguvu za upanga, wakati wa msiba wao, wakati wa mwisho wa uovu. 6 Basi, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, nitakuweka tayari kwa damu, na damu itakufuatia; ikiwa hukuchukia damu, basi damu itakufuatia. 7 Hivyo ndivyo nitakavyoufanya mlima Seiri kuwa ajabu na ukiwa; nami nitakatilia mbali nao mtu apitaye, na mtu arejeaye. 8 Nami nitaijaza milima yake watu wake waliouawa; katika milima yako, na katika mabonde yako, na katika mifereji yako ya maji yote, wataanguka wao watakaouawa kwa upanga. 9 Nitakufanya kuwa ukiwa wa daima, na miji yako haitakaliwa na watu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 10 Kwa sababu umesema, Mataifa haya mawili na nchi hizi mbili zitakuwa zangu, nasi tutazimiliki, ijapokuwa Bwana alikuwako huko. 11 Basi, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, nitatenda kwa kadiri ya hasira yako, na kwa kadiri ya wivu wako, ulioudhihirisha kwa kuwachukia; nami nitajidhihirisha kwao, nitakapokuhukumu wewe. 12 Nawe utajua ya kuwa mimi, Bwana, nimeyasikia matukano yako yote, uliyoyanena juu ya milima ya Israeli, ukisema, Wamefanyika ukiwa, wametiwa katika mikono yetu tuwale. 13 Nanyi mmejitukuza juu yangu kwa vinywa vyenu, na kuyaongeza maneno juu yangu; nimesikia mimi. 14 Bwana MUNGU asema hivi; Dunia yote itakapofurahi, nitakufanya kuwa ukiwa. 15 Kama vile ulivyofurahi juu ya urithi wa nyumba ya Israeli, kwa sababu ilikuwa ukiwa, ndivyo nitakavyokutenda wewe; utakuwa ukiwa, Ee mlima Seiri, na Edomu yote, naam, yote pia; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 36

1 Na wewe, mwanadamu, itabirie milima ya Israeli, useme, Enyi milima ya Israeli, lisikieni neno la Bwana. 2 Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu adui amesema juu yenu, Aha! Na, Mahali pa juu pa zamani pamekuwa petu tupamiliki; 3 basi tabiri useme, Bwana MUNGU asema hivi; Kwa sababu, naam, kwa sababu wamewafanya ninyi kuwa ukiwa, na kuwameza pande zote, mpate kuwa milki kwa mabaki ya mataifa, nanyi mmeambwa kwa midomo yao waongeao, na kwa masingizio ya watu; 4 kwa sababu hiyo, enyi milima ya Israeli, lisikieni neno la Bwana MUNGU; Bwana MUNGU aiambia hivi hiyo milima na vilima, mifereji ya maji na mabonde, mahali palipoharibika na kuwa ukiwa, na miji iliyoachwa na watu, ambayo imekuwa mateka, na kuzomewa na mabaki ya mataifa, walio karibu pande zote; 5 basi Bwana MUNGU asema hivi; Hakika kwa moto wa wivu wangu nimenena juu ya mabaki ya mataifa, na juu ya Edomu yote, waliojiandikia nchi yangu kuwa milki yao, kwa furaha ya mioyo yao yote, kwa jeuri ya roho zao, ili waitupe nje kuwa mawindo; 6 basi katika kutabiri habari za nchi ya Israeli, uiambie milima na vilima, mifereji ya maji na mabonde, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nimenena katika wivu wangu na hasira yangu, kwa sababu mmechukua aibu ya mataifa; 7 basi Bwana MUNGU asema hivi; Nimeinua mkono wangu, kusema, Hakika, mataifa walio karibu nanyi pande zote, wao watachukua aibu yao. 8 Lakini ninyi, enyi milima ya Israeli, mtachipuza matawi yenu na kuwapa watu wangu Israeli matunda yenu; maana wa karibu kuja. 9 Maana, tazama, mimi nasimama upande wenu, nami nitawaelekea, nanyi mtalimwa na kupandwa mbegu; 10 nami nitaongeza watu juu yenu, nyumba yote ya Israeli, naam, yote pia; nayo miji itakaliwa na watu, na mahali palipoharibika patajengwa. 11 Nami nitaongeza juu yenu mwanadamu na mnyama, nao watazidi na kuzaa; nami nitawakalisha watu ndani yenu, kwa kadiri ya hali yenu ya kwanza, nami nitawatendea mema kuliko mema ya mianzo yenu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 12 Naam, nitaleta watu watembee juu yenu, naam, watu wangu Israeli; nao watakumiliki, nawe utakuwa urithi wao, wala hutawafisha watoto wao tena tangu leo. 13 Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa watu hukuambia, wewe nchi u mwenye kula watu, nawe umekuwa mwenye kufisha watu wa taifa lako; 14 basi hutakula watu tena, wala hutafisha watu wa taifa lako tena, asema Bwana MUNGU; 15 wala sitakusikizisha tena aibu yao wasioamini, wala hutachukua matukano ya watu tena; wala hutalikwaza taifa lako tena, asema Bwana MUNGU. 16 Tena, neno la Bwana likanijia, kusema, 17 Mwanadamu, nyumba ya Israeli walipokaa katika nchi yao wenyewe, waliitia uchafu kwa njia yao na kwa matendo yao. Njia yao mbele zangu ilikuwa kama uchafu wa mwanamke wakati wa kutengwa kwake. 18 Kwa hiyo nalimwaga hasira yangu juu yao, kwa ajili ya damu waliyoimwaga juu ya nchi, na kwa sababu wameitia uchafu kwa vinyago vyao. 19 Nikawatawanya katika mataifa, wakatapanyika katika nchi nyingi; kwa kadiri ya njia yao, na kwa kadiri ya matendo yao, naliwahukumu. 20 Nao walipoyafikilia mataifa yale waliyoyaendea, walilitia unajisi jina langu takatifu; kwa kuwa watu waliwanena, wakisema, Watu hawa ni watu wa Bwana, nao wametoka katika nchi yake. 21 Lakini, naliwahurumia kwa ajili ya jina langu takatifu, ambalo nyumba ya Israeli walikuwa wamelitia unajisi katika mataifa waliyoyaendea. 22 Kwa hiyo; waambieni nyumba ya Israeli, Bwana MUNGU asema hivi Sitendi hili kwa ajili yenu, Ee nyumba ya Israeli, bali kwa ajili ya jina langu takatifu, mlilolitia unajisi katika mataifa mliyoyaendea. 23 Nami nitalitakasa jina langu kuu, lililotiwa unajisi katika mataifa, mlilolitia unajisi kati yao; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, asema Bwana MUNGU, nitakapotakaswa kati yenu mbele ya macho yao. 24 Maana nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe. 25 Nami nitawanyunyizia maji safi, nanyi mtakuwa safi; nitawatakaseni na uchafu wenu wote, na vinyago vyenu vyote. 26 Nami nitawapa ninyi moyo mpya, nami nitatia roho mpya ndani yenu, nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani ya mwili wenu, nami nitawapa moyo wa nyama. 27 Nami nitatia roho yangu ndani yenu, na kuwaendesha katika sheria zangu, nanyi mtazishika hukumu zangu, na kuzitenda. 28 Nanyi mtakaa katika nchi ile niliyowapa baba zenu, nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. 29 Nami nitawaokoeni na uchafu wenu wote; nitaiita ngano, na kuiongeza, wala sitaweka njaa juu yenu tena. 30 Nami nitazidisha matunda ya miti, na mazao ya mashamba, msipate tena kutukanwa na mataifa kwa sababu ya njaa. 31 Ndipo mtazikumbuka njia zenu mbaya, na matendo yenu yasiyokuwa mema, nanyi mtajichukia nafsi zenu kwa macho yenu, kwa sababu ya maovu yenu na machukizo yenu. 32 Ijulikane kwenu ya kuwa silitendi neno hili kwa ajili yenu, asema Bwana MUNGU; tahayarikeni, na kufadhaika, kwa sababu ya njia zenu, Enyi nyumba ya Israeli. 33 Bwana MUNGU asema hivi; Siku ile nitakapowatakaseni na maovu yenu yote, nitaifanya miji ikaliwe na watu, na palipobomolewa pajengwe tena. 34 Nchi iliyokuwa ukiwa italimwa, ijapokuwa ilikuwa ukiwa mbele ya macho ya watu wote waliopita. 35 Nao watasema, Nchi hii, iliyokuwa ukiwa, imekuwa kama bustani ya Adeni; nayo miji iliyokuwa mahame, na ukiwa, na magofu, sasa ina maboma, inakaliwa na watu. 36 Ndipo mataifa, waliobaki karibu yenu pande zote, watajua ya kuwa mimi, Bwana, nimejenga mahali palipoharibika, nami nimepanda mbegu katika nchi iliyokuwa ukiwa; mimi, Bwana, nimesema hayo; tena nitayatenda. 37 Bwana MUNGU asema hivi, Tena kwa ajili ya jambo hili nitaulizwa na nyumba ya Israeli, ili niwatendee; nami nitawaongeza kwa watu kama kundi la kondoo. 38 Kama kundi lililo tayari kutolewa sadaka, kama kundi la Yerusalemu katika sikukuu zake zilizoamriwa; ndivyo itakavyojazwa watu, miji ile iliyokuwa maganjo; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 37

1 Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; 2 akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana. 3 Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe. 4 Akaniambia tena, Toa unabii juu ya mifupa hii, uiambie, Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la Bwana. 5 Bwana MUNGU aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi. 6 Nami nitatia mishipa juu yenu, nami nitaleta nyama iwe juu yenu, na kuwafunika ngozi, na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 7 Basi nikatoa unabii kama nilivyoamriwa; hata nilipokuwa nikitoa unabii, palikuwa na mshindo mkuu; na tazama, tetemeko la nchi, na ile mifupa ikasogeleana, mfupa kwa mfupa mwenziwe. 8 Nikatazama, kumbe! Kulikuwa na mishipa juu yake, nyama ikatokea juu yake, ngozi ikaifunika juu yake; lakini haikuwamo pumzi ndani yake. 9 Ndipo akaniambia, Tabiri, utabirie upepo, mwanadamu, ukauambie upepo, Bwana MUNGU asema hivi; Njoo, kutoka pande za pepo nne, Ee pumzi, ukawapuzie hawa waliouawa, wapate kuishi. 10 Basi nikatabiri kama alivyoniamuru; pumzi ikawaingia, wakaishi, wakasimama kwa miguu yao, jeshi kubwa mno. 11 Kisha akaniambia, Mwanadamu, mifupa hii ni nyumba yote ya Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea; tumekatiliwa mbali kabisa. 12 Basi tabiri, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli. 13 Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu. 14 Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimesema hayo, na kuyatimiza, asema Bwana. 15 Neno la Bwana likanijia tena, kusema, 16 Na wewe mwanadamu, twaa kijiti kimoja; ukaandike juu yake, Kwa Yuda, na kwa wana wa Israeli wenzake; kisha, twaa kijiti cha pili; ukaandike juu yake, Kwa Yusufu, kijiti cha Efraimu, na kwa nyumba yote ya Israeli wenzake; 17 ukaviunge pamoja kwa ajili yako hiki na hiki viwe kijiti kimoja, viwe kimoja katika mkono wako. 18 Na wana wa watu wangu watakapokuambia, wakisema, Je! Hutatuonyesha maana ya mambo hayo utendayo? 19 Waambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitakitwaa kijiti cha Yusufu, kilicho mkononi mwa Efraimu, na kabila za Israeli wenzake, nami nitawaweka pamoja nacho, yaani, pamoja na kijiti cha Yuda, na kuvifanya kuwa kijiti kimoja; navyo vitakuwa kimoja mkononi mwangu. 20 Navyo vijiti, ambavyo uliandika juu yake, vitakuwa mkononi mwako mbele ya macho yao. 21 Ukawaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitawatwaa wana wa Israeli toka kati ya mataifa walikokwenda, nami nitawakusanya pande zote, na kuwaleta katika nchi yao wenyewe; 22 nami nitawafanya kuwa taifa moja katika nchi hiyo, juu ya milima ya Israeli; na mfalme mmoja atakuwa mfalme wao wote; wala hawatakuwa tena mataifa mawili, wala hawatagawanyikana kuwa falme mbili tena, hata milele. 23 Wala hawatajitia uchafu tena kwa vinyago vyao, wala kwa vitu vyao vichukizavyo, wala kwa makosa yao mojawapo; lakini nitawaokoa, na kuwatoa katika makao yao yote, ambayo wamefanya dhambi ndani yake, nami nitawatakasa; basi watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao. 24 Na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mfalme juu yao, nao wote watakuwa na mchungaji mmoja; nao wataenenda katika hukumu zangu, na kuzishika amri zangu, na kuzitenda. 25 Nao watakaa katika nchi niliyompa Yakobo, mtumishi wangu, walimokaa baba zenu; nao watakaa humo, wao na watoto wao, na watoto wa watoto wao, milele; na Daudi, mtumishi wangu, atakuwa mkuu wao milele. 26 Tena nitafanya agano la amani pamoja nao; litakuwa agano la milele pamoja nao; nami nitawaweka na kuwazidisha, na patakatifu pangu nitapaweka katikati yao milele. 27 Tena maskani yangu itakuwa pamoja nao; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. 28 Na mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, mimi niwatakasaye Israeli, patakatifu pangu patakapokuwa katikati yao milele.

Ezekieli 38

1 Neno la Bwana likanijia, kusema, 2 Mwanadamu, kaza uso wako, umwelekee Gogu, wa nchi ya Magogu, mkuu wa Roshi, Mesheki, na Tubali, ukatabiri juu yake, 3 useme, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ewe Gogu, mkuu wa Roshi, na Mesheki, na Tubali; 4 nami nitakugeuza na kutia kulabu katika mataya yako, nami nitakutoa, pamoja na jeshi lako lote, farasi na hao wapandao farasi, wote wamevaa silaha za namna zote, jeshi kubwa sana, wenye ngao na kigao, wote wakishika upanga; 5 Uajemi, na Kushi, na Putu, pamoja nao; wote wana ngao na chapeo; 6 Gomeri, na vikosi vyake vyote; nyumba ya Togarma, pande za mwisho za kaskazini, na vikosi vyake vyote; naam, watu wengi pamoja nawe. 7 Ujiweke tayari, naam, jiweke tayari, wewe na majeshi yako yote waliokukusanyikia, nawe uwe jemadari wao. 8 Na baada ya siku nyingi utajiliwa; katika miaka ya mwisho, utaingia nchi iliyorudishiwa hali yake ya kwanza, baada ya kupigwa kwa upanga, iliyokusanywa toka kabila nyingi za watu, juu ya milima ya Israeli, iliyokuwa ukiwa wa daima; lakini imetolewa katika kabila za watu, nao watakaa salama salimini wote pia. 9 Nawe utapaa juu, utakuja kama tufani, utakuwa kama wingu kuifunika nchi, wewe, na vikosi vyako vyote, na kabila nyingi za watu pamoja nawe. 10 Bwana MUNGU asema hivi; Itakuwa katika siku hiyo, mawazo yataingia moyoni mwako, nawe utakusudia kusudi baya; 11 nawe utasema, Nitapanda juu niiendee nchi yenye vijiji visivyo na maboma; nitawaendea watu wanaostarehe, wanaokaa salama, wote wakikaa pasipo kuta, ambao hawana makomeo wala malango; 12 ili kuteka mateka, na kuwinda mawindo; uugeuze mkono wako juu ya mahali palipoharibika, ambapo sasa panakaliwa na watu, na juu ya watu waliokusanyika toka mataifa, waliopata ng'ombe na mali, wakaao katikati ya dunia. 13 Sheba, na Dedani, na wafanya biashara wa Tarshishi, pamoja na wana-simba wake wote, watakuambia, Je! Umekuja kuteka mateka? Umekusanya jeshi lako, ili kuwinda mawindo? Kuchukua fedha na dhahabu, kuchukua ng'ombe na mali, kuteka mateka mengi sana? 14 Basi, mwanadamu, tabiri, umwambie Gogu, Bwana MUNGU asema hivi; Katika siku ile watu wangu, Israeli, watakapokaa salama, hutapata habari? 15 Nawe utakuja kutoka mahali pako, kutoka pande za mwisho za kaskazini, wewe, na watu wa kabila nyingi pamoja nawe, wote wamepanda farasi, kusanyiko kubwa, na jeshi kuu; 16 nawe utapanda juu uwajilie watu wangu, Israeli, kama wingu kuifunika nchi; itakuwa katika siku za mwisho, nitakuleta upigane na nchi yangu, ili mataifa wanijue, nitakapotakaswa kwako, Ewe Gogu, mbele ya macho yao. 17 Bwana MUNGU asema hivi; Je! Wewe ndiwe niliyemnena zamani za kale, kwa vinywa vya watumishi wangu, manabii wa Israeli, waliotabiri siku zile kwa muda wa miaka mingi, ya kwamba nitakuleta upigane nao? 18 Itakuwa katika siku hiyo, Gogu atakapokuja kupigana na nchi ya Israeli, asema Bwana MUNGU, ghadhabu yangu itapanda katika mianzi ya pua yangu. 19 Kwa maana katika wivu wangu, na katika moto wa ghadhabu yangu, nimenena, Hakika katika siku ile kutakuwako tetemeko kubwa katika nchi ya Israeli; 20 hata samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama wa kondeni, na vitu vyote vitambaavyo juu ya nchi, na wanadamu wote walio juu ya uso wa nchi, watatetemeka mbele ya uso wangu; nayo milima itatupwa chini, na magenge yataanguka, na kila ukuta utaanguka chini. 21 Nami nitaita upanga, uje juu yake katika milima yangu yote, asema Bwana MUNGU; nao upanga wa kila mtu utakuwa juu ya ndugu yake. 22 Nami nitamhukumu kwa tauni, na kwa damu; nami nitanyesha mvua ifurikayo, na mvua ya mawe makubwa sana, na moto na kiberiti juu yake, na vikosi vyake, na watu wa kabila nyingi walio pamoja naye. 23 Nami nitajitukuza, na kujitakasa, na kujidhihirisha, mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Ezekieli 39

1 Na wewe, mwanadamu, tabiri juu ya Gogu, useme, Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, mimi ni juu yako, Ewe Gogu, mkuu wa Roshi, Mesheki, na Tubali; 2 nami nitakugeuza na kukuongoza, nami nitakupandisha toka pande za mwisho za kaskazini; nami nitakuleta juu ya milima ya Israeli; 3 nami nitaupiga upinde wako, utoke katika mkono wako wa kushoto, na mishale yako nitaiangusha, itoke katika mkono wako wa kulia. 4 Utaanguka juu ya milima ya Israeli, wewe, na vikosi vyako vyote, na watu wa kabila nyingi walio pamoja nawe; nami nitakutoa na kuwapa ndege wa kila namna walao nyama, na wanyama wa nchi, uliwe na wao. 5 Utaanguka katika uwanda; kwa maana mimi nimenena neno hili, asema Bwana MUNGU. 6 Nami nitapeleka moto juu ya Magogu; na juu ya watu wote wakaao salama katika visiwa; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. 7 Na jina langu takatifu nitalifanya kuwa limejulika kati ya watu wangu Israeli; wala sitaliacha jina langu takatifu kutiwa unajisi tena; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, na Aliye Mtakatifu katika Israeli. 8 Tazama, linakuja, nalo litatendeka, asema Bwana MUNGU; hii ndiyo siku ile niliyoinena. 9 Hao wakaao katika miji ya Israeli watatoka, nao watafanya mioto kwa silaha za vita na kuziteketeza, ngao, na vigao, na pinde, na mishale, na mafumo, na mikuki, nao watazitumia kama kuni kwa muda wa miaka saba; 10 hata hawataokota kuni mashambani, wala hawatakata kuni msituni; maana watafanya mioto kwa silaha zile; nao watawateka nyara watu waliowateka wao, na kunyang'anya vitu vya watu walionyang'anya vitu vyao, asema Bwana MUNGU. 11 Tena, itakuwa katika siku hiyo, nitampa Gogu pa kuzikia katika Israeli, bonde la wapitao, upande wa mashariki wa bahari; nalo litawazuia wapitao; na huko watamzika Gogu na watu wake jamii yote; nao wataliita, Bonde la Hamon-Gogu. 12 Na kwa muda wa miezi saba nyumba ya Israeli watakuwa wakiwazika, wapate kuisafisha nchi. 13 Naam, watu wote wa nchi hiyo watawazika; itakuwa ni sifa kwao katika siku ile nitakapotukuzwa, asema Bwana MUNGU. 14 Nao watawachagua watu wa kufanya kazi ya daima, watakaopita kati ya nchi, ili kuwazika waliosalia juu ya uso wa nchi, ili kuisafisha; miezi saba itakapokwisha kupita watatafuta. 15 Na hao wapitao kati ya nchi watatafuta; na mtu ye yote aonapo mfupa wa mtu, ndipo atakapoweka alama karibu nao, hata wazishi watakapouzika katika bonde la Hamon- Gogu. 16 Tena, Hamona litakuwa jina la mji. Hivyo ndivyo watakavyosafisha nchi. 17 Na wewe, mwanadamu, Bwana MUNGU asema hivi; Sema na ndege wa kila namna, na kila mnyama wa kondeni, Jikusanyeni, mje; jikusanyeni pande zote mwijilie sadaka yangu niifanyayo kwa ajili yenu, naam, sadaka kubwa juu ya milima ya Israeli, mpate kula nyama na kunywa damu. 18 Mtakula nyama yao walio hodari, na kunywa damu ya wakuu wa dunia, ya kondoo waume na ya wana-kondoo, na ya mbuzi, na ya ng'ombe, wote na wanono wa Bashani. 19 Nanyi mtakula mafuta na kushiba, mtakunywa damu na kulewa, na sadaka yangu niliyoifanya kwa ajili yenu. 20 Nanyi mtashibishwa mezani pangu kwa farasi, na magari ya vita, na mashujaa, na watu wote wa vita, asema Bwana MUNGU. 21 Nami nitauweka utukufu wangu kati ya mataifa, na mataifa wote wataiona hukumu yangu niliyoitekeleza, na mkono wangu niliouweka juu yao. 22 Basi, nyumba ya Israeli watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wao, tangu siku hiyo na baadaye. 23 Nao mataifa watajua ya kuwa nyumba ya Israeli walihamishwa, na kwenda kifungoni, kwa sababu ya uovu wao; kwa sababu waliniasi, nami nikawaficha uso wangu; basi nikawatia katika mikono ya adui zao, nao wakaanguka kwa upanga, wote pia. 24 Kwa kadiri ya uchafu wao, kwa kadiri ya makosa yao, ndivyo nilivyowatenda, nami nikawaficha uso wangu. 25 Kwa sababu hiyo, Bwana MUNGU asema hivi, Sasa nitawarejeza watu wa Yakobo waliohamishwa, nitawahurumia nyumba yote ya Israeli; nami nitalionea wivu jina langu takatifu. 26 Nao watachukua aibu yao, na makosa yao yote waliyoniasi, watakapokaa salama katika nchi yao wenyewe, wala hapana mtu atakayewatia hofu; 27 nitakapokuwa nimewaleta tena kutoka kabila za watu, na kuwakusanya kwa kuwatoa katika nchi za adui zao, na kutakaswa kati yao mbele ya macho ya mataifa mengi. 28 Nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wao, kwa kuwa naliwahamisha, waende utumwani kati ya mataifa, na mimi nikawakusanya, na kuwaingiza katika nchi yao wenyewe; wala sitawaacha tena huko kamwe, hata mmojawapo; 29 wala sitawaficha uso wangu tena; kwa maana nimemwaga roho yangu juu ya nyumba ya Israeli, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 40

1 Katika mwaka wa ishirini na tano wa kuhamishwa kwetu, mwanzo wa mwaka, siku ya kumi ya mwezi, katika mwaka wa kumi na nne baada ya kupigwa mji, siku iyo hiyo, mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, akanileta huko. 2 Katika maono ya Mungu alinileta mpaka nchi ya Israeli, akaniweka juu ya mlima mrefu sana, ambao juu yake palikuwapo kana kwamba ni umbo la mji upande wa kusini. 3 Akanileta huko, na tazama, alikuwapo mtu, ambaye kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwa shaba, naye alikuwa na uzi wa kitani mkononi mwake, na mwanzi wa kupimia; akasimama karibu na lango. 4 Mtu yule akaniambia, Mwanadamu, tazama kwa macho yako, sikia kwa masikio yako, ukaweke moyoni mwako, yote nitakayokuonyesha; maana umeletwa hapa kusudi nikuonyeshe haya; tangaza habari ya yote utakayoyaona kwa nyumba ya Israeli. 5 Na, tazama, kulikuwa na ukuta nje ya nyumba pande zote, na katika mkono wa mtu yule mwanzi wa kupimia, urefu wake dhiraa sita, kila dhiraa, dhiraa na shubiri; basi akaupima upana wa jengo lile, mwanzi mmoja, na urefu wake, mwanzi mmoja. 6 Kisha akaenda mpaka lango lielekealo upande wa mashariki, akapanda madaraja yake; akakipima kizingiti cha lango; upana wake mwanzi mmoja; na kizingiti cha pili, upana wake mwanzi mmoja. 7 Na kila chumba, upana wake mwanzi mmoja, na urefu wake mwanzi mmoja; na nafasi iliyokuwa kati ya vyumba ni dhiraa tano; na kizingiti cha lango lililokuwa karibu na ukumbi wa lango lililoielekea nyumba, mwanzi mmoja. 8 Akaupima na ukumbi wa lango lililoielekea nyumba, mwanzi mmoja. 9 Kisha akaupima ukumbi wa lango, dhiraa nane; na miimo yake, dhiraa mbili; na ukumbi wa lango uliielekea nyumba. 10 Na vyumba vya walinzi, vya lango upande wa mashariki, vilikuwa vitatu upande huu, na vitatu upande huu; vyote vitatu vya kipimo kimoja; nayo miimo ilikuwa na kipimo kimoja, upande huu na upande huu. 11 Akaupima upana wa mahali pa kuliingilia lango, dhiraa kumi; na urefu wa lango, dhiraa kumi na tatu. 12 Na mpaka, mbele ya vile vyumba, dhiraa moja upande huu, na mpaka, dhiraa moja upande huu; na vile vyumba, dhiraa sita upande huu, na dhiraa sita upande huu. 13 Akalipima lango, toka paa la chumba kimoja hata paa la chumba cha pili, upana wa dhiraa ishirini na tano; mlango mmoja ukielekea mlango wa pili. 14 Akafanya miimo pia, dhiraa sitini; na uwanda uliufikilia mwimo, lango lile likizungukwa pande zote. 15 Na toka mahali palipo mbele ya lango, penye maingilio yake, hata mahali palipo mbele ya ukumbi wa ndani ya lango, dhiraa hamsini. 16 Na kwa vile vyumba palikuwa na madirisha yaliyofungwa, na kwa miimo yake ndani ya lango pande zote, na kwa matao yake vivyo hivyo; na madirisha yalikuwako, pande zote upande wa ndani, tena palikuwa na mitende juu ya kila mwimo. 17 Ndipo akanileta mpaka ua wa nje, na tazama, palikuwa na vyumba, na sakafu iliyofanyizwa kwa ule ua pande zote; vyumba thelathini vilikuwako juu ya sakafu ile. 18 Na ile sakafu ilikuwa kando ya malango, urefu wake sawasawa na urefu wa malango, yaani, sakafu ya chini. 19 Kisha akaupima upana, toka mahali palipokuwa mbele ya lango la chini hata mahali palipokuwa mbele ya ua wa ndani, nje yake, dhiraa mia upande wa mashariki, na upande wa kaskazini. 20 Nalo lango la ua wa nje, lililoelekea kaskazini, akalipima urefu wake, na upana wake. 21 Na vyumba vyake vya walinzi vilikuwa vitatu upande huu, na vitatu upande huu; na miimo yake, na matao yake, kipimo chake ni sawasawa na kipimo cha lango la kwanza; urefu wake dhiraa hamsini, na upana wake dhiraa ishirini na tano. 22 Na madirisha yake, na matao yake, na mitende yake, kipimo chake ni sawasawa na kipimo cha lango lililoelekea upande wa mashariki; nao hupanda kwa madaraja saba; na matao yake yalikuwa mbele yake. 23 Na ule ua wa ndani ulikuwa na lango lililoelekea lile lango la pili, upande wa kaskazini, na upande wa mashariki; akapima toka lango hata lango, dhiraa mia. 24 Akanileta mpaka upande wa kusini, na tazama, lango lililoelekea kusini; akaipima miimo yake, na matao yake, sawasawa na vipimo hivyo. 25 Tena palikuwa na madirisha ndani yake, na katika matao yake pande zote kama madirisha hayo; urefu wake dhiraa hamsini, na upana wake dhiraa ishirini na tano. 26 Tena palikuwa na madaraja saba ya kulipandia, na matao yake yalikuwa mbele yake; nalo lilikuwa na mitende, mmoja upande huu, na mmoja upande huu, juu ya miimo yake. 27 Tena ua wa ndani ulikuwa na lango, lililoelekea kusini; akapima toka lango hata lango, kwa kuelekea upande wa kusini, dhiraa mia. 28 Kisha akanileta mpaka ua wa ndani karibu na lango lililoelekea kusini; akalipima lango la kusini kwa vipimo vivyo hivyo; 29 navyo vyumba vyake vya walinzi, na miimo yake, na matao yake, sawasawa na vipimo hivyo; tena palikuwa na madirisha ndani yake, na katika matao yake pande zote; urefu wake dhiraa hamsini, na upana wake dhiraa ishirini na tano. 30 Tena palikuwa na matao pande zote, urefu wake dhiraa ishirini na tano na upana wake dhiraa tano. 31 Na matao yake yaliuelekea ua wa nje, na mitende ilikuwa juu ya miimo yake; palikuwa na madaraja manane ya kuupandia. 32 Akanileta mpaka ua wa ndani ulioelekea upande wa mashariki, akalipima lango kwa vipimo vivyo hivyo; 33 navyo vyumba vyake vya walinzi, na miimo yake, na matao yake, kwa vipimo hivyo; tena palikuwa na madirisha ndani yake, na katika matao yake pande zote; urefu wake dhiraa hamsini, na upana wake dhiraa ishirini na tano. 34 Na matao yake yaliuelekea ua wa nje; na mitende ilikuwa juu ya miimo yake, upande huu na upande huu; tena palikuwa na madaraja manane ya kuupandia. 35 Akanileta mpaka lango lililoelekea upande wa kaskazini; akalipima kwa vipimo vivyo hivyo; 36 vyumba vyake vya walinzi, na miimo yake, na matao yake; tena palikuwa na madirisha ndani yake pande zote; urefu wake dhiraa hamsini, na upana wake dhiraa ishirini na tano. 37 Na miimo yake iliuelekea ua wa nje; na mitende ilikuwa juu ya miimo yake, upande huu na upande huu; tena palikuwa na madaraja manane ya kuupandia. 38 Na chumba, pamoja na lango lake, kilikuwa karibu na miimo ya malango; ndiko walikoiosha sadaka ya kuteketezwa. 39 Na katika ukumbi wa lango palikuwa na meza mbili upande huu, na meza mbili upande huu, ili kuichinja sadaka ya kuteketezwa, na sadaka ya dhambi, na sadaka ya hatia. 40 Na upande mmoja, nje, penye madaraja ya kuliingia lango lililoelekea kaskazini, palikuwa na meza mbili; na upande wa pili, ulio wa ukumbi wa lango hilo, palikuwa na meza mbili. 41 Palikuwa na meza nne upande huu, na meza nne upande huu, karibu na lango; meza nane ambazo juu yake walizichinja sadaka. 42 Tena palikuwa na meza nne kwa sadaka za kuteketezwa, za mawe yaliyochongwa; urefu wake dhiraa moja na nusu, na upana wake dhiraa moja na nusu, na kimo chake dhiraa moja; juu yake waliviweka vyombo vya kuchinjia sadaka za kuteketezwa na sadaka. 43 Tena hizo kulabu, ambazo urefu wake ni shubiri, zilifungwa ndani pande zote; na juu ya meza hizo ilikuwako nyama ya matoleo. 44 Tena nje ya lango la ndani palikuwa na vyumba kwa waimbaji, katika ua wa ndani, uliokuwa kando ya lango lililoelekea kaskazini, navyo vilikabili upande wa kusini; na kimoja kando ya lango lililoelekea upande wa mashariki, kilikabili upande wa kaskazini. 45 Akaniambia, Chumba hiki kinachokabili upande wa kusini ni kwa makuhani, yaani, hao walinzi wa malindo ya nyumba. 46 Nacho chumba kinachokabili upande wa kaskazini ni kwa makuhani, walinzi wa malindo ya madhabahu; hao ni wana wa Sadoki, ambao miongoni mwa wana wa Lawi wamkaribia Bwana, ili kumtumikia. 47 Akaupima huo ua, na urefu wake ulikuwa dhiraa mia, na upana wake dhiraa mia, mraba; nayo dhabahu ilikuwa mbele ya nyumba. 48 Ndipo akanileta mpaka ukumbi wa nyumba, akapima kila mwimo wa ukumbi, dhiraa tano upande huu, na dhiraa tano upande huu; na upana wa lango ulikuwa dhiraa tatu upande huu, na dhiraa tatu upande huu. 49 Urefu wa ukumbi ulikuwa dhiraa ishirini, na upana wake dhiraa kumi na moja; karibu na madaraja ambayo waliupandia; tena palikuwa na nguzo karibu na miimo, moja upande huu, na moja upande huu.

Ezekieli 41

1 Akanileta mpaka hekaluni, akaipima miimo, upana wake dhiraa sita upande mmoja, na upana wake dhiraa sita upande wa pili, ambao ulikuwa ni upana wa maskani. 2 Na upana wa maingilio yake ulikuwa dhiraa kumi; na mbavu za maingilio zilikuwa dhiraa tano upande huu, na dhiraa tano upande huu; akaupima urefu wake, dhiraa arobaini, na upana wake, dhiraa ishirini. 3 Kisha akaingia ndani, akapima kila mwimo wa maingilio, dhiraa mbili; nayo maingilio, dhiraa sita; na upana wa maingilio dhiraa saba. 4 Akaupima urefu wake; dhiraa ishirini, na upana wake, dhiraa ishirini, mbele ya hekalu; akaniambia, Hapa ndipo mahali patakatifu kuliko kila mahali. 5 Kisha akaupima ukuta wa nyumba, dhiraa sita; na upana wa kila chumba cha mbavuni, dhiraa nne, kuizunguka nyumba pande zote. 6 Na vile vyumba vya mbavuni vilikuwa na orofa tatu, moja juu ya mwenziwe; vilikuwa thelathini, safu baada ya safu; navyo viliingia ndani ya ukuta uliokuwa wa nyumba, kwa vile vyumba vya mbavuni pande zote vipate kushikamana nao, wala visishikamane na ukuta wa nyumba. 7 Na vile vyumba vya mbavuni vilizidi kuwa vipana, kwa kadiri vilivyoizunguka nyumba juu kwa juu; maana kule kuzunguka kwake kulikwenda juu kwa juu, kuizunguka nyumba; basi upana wa nyumba ulikuwa ule ule hata juu; basi hupanda juu toka chumba cha chini hata chumba cha juu, kwa njia ya kile chumba cha katikati. 8 Tena, nikaona ya kwamba nyumba ile ilikuwa na sakafu ya mawe, iliyoinuliwa pande zote; nayo misingi ya vyumba vya mbavuni ilikuwa mwanzi mzima wa dhiraa sita. 9 Unene wa ukuta uliokuwa wa vile vyumba vya mbavuni, upande wa nje, ulikuwa dhiraa tano; nayo nafasi iliyobaki ilikuwa dhiraa tano; na kati ya vyumba vya mbavuni vya nyumba, 10 na vyumba vya walinzi, upana wa dhiraa ishirini, kuizunguka nyumba pande zote. 11 Na milango ya vile vyumba vya mbavuni iliielekea nafasi ile iliyobaki, mlango mmoja ulielekea upande wa kaskazini, na mlango mmoja upande wa kusini; na upana wa nafasi iliyobaki ulikuwa dhiraa tano pande zote. 12 Nalo jengo lililokabili mahali palipotengeka upande wa magharibi, upana wake dhiraa sabini; na ukuta wa lile jengo, unene wake dhiraa tano pande zote, na urefu wake dhiraa tisini. 13 Basi akaipima nyumba, urefu wake dhiraa mia; na mahali pale palipotengeka na jengo lile, pamoja na kuta zake, urefu wake dhiraa mia; 14 tena upana wa uso wa nyumba, na wa mahali palipotengeka upande wa mashariki, dhiraa mia. 15 Akaupima urefu wa jengo lile lililokabili mahali palipotengeka, palipokuwa nyuma yake, na baraza zake upande huu na upande huu, dhiraa mia; na hekalu la ndani, na kumbi za ua; 16 na vizingiti, na madirisha yaliyofungwa, na baraza za pande zote za orofa zile tatu, zilizokikabili kizingiti, zilitiwa mabamba ya mti pande zote; na toka chini hata madirishani; (nayo madirisha yamefunikwa); 17 na mpaka juu ya mlango hata nyumba ya ndani, na nje, na juu ya kuta zote pande zote, katika nyumba ya ndani, na ya nje, 18 kulipambwa kwa makerubi na mitende; mtende mmoja kati ya kerubi na kerubi, na kila kerubi lilikuwa na nyuso mbili; 19 basi palikuwa na uso wa mwanadamu kuelekea mtende mmoja, na uso wa mwana-simba kuelekea mtende wa pili; ndivyo vilivyofanyika katika nyumba nzima pande zote. 20 Toka chini hata juu ya mlango makerubi yamefanyika, na mitende, na vivi hivi ukuta wa hekalu. 21 Na hilo hekalu, miimo ya milango yake ilikuwa ya miraba; na mbele ya patakatifu kuonekana kwake palionekana kama hapo kwanza. 22 Madhabahu ilikuwa ni ya miti, kimo chake dhiraa tatu, na urefu wake dhiraa mbili; na pembe zake, na msingi wake, na kuta zake zilikuwa za miti; akaniambia, Hii ndiyo meza iliyo mbele za Bwana. 23 Nalo hekalu na patakatifu palikuwa na milango miwili. 24 Na milango hiyo, kila mmoja ulikuwa na mbao mbili; mbao mbili zigeukazo; mbao mbili za mlango mmoja, na mbao mbili za mlango wa pili. 25 Na milango ya hekalu ilifanyiziwa makerubi na mitende vile vile, kama zile kuta zilivyofanyiziwa; tena palikuwa na boriti nene juu ya uso wa ukumbi, nje. 26 Tena palikuwa na madirisha yaliyofungwa, na mitende, upande huu na upande huu, katika pande za ukumbi; ndiyo habari ya vyumba vya mbavuni vya nyumba hiyo, na vya boriti zile nene.

Ezekieli 42

1 Ndipo akanileta mpaka ua wa nje, njia ya kuelekea upande wa kaskazini; akaniingiza katika chumba kilichopakabili mahali palipotengeka, na kilicholikabili jengo upande wa kaskazini; 2 kukabili urefu wa dhiraa mia palikuwa na mlango wa kaskazini, na upana wake ni dhiraa hamsini. 3 Kukabili zile dhiraa ishirini za ua wa ndani, na kukabili sakafu ya mawe ya ua wa nje, palikuwa na baraza kukabili baraza katika orofa ya tatu. 4 Na mbele ya vile vyumba palikuwa na njia, upana wake dhiraa kumi upande wa ndani, njia ya dhiraa mia, na milango yake ilielekea upande wa kaskazini. 5 Basi vile vyumba vya juu vilikuwa vifupi zaidi; kwa maana baraza zile zilivipunguza kuliko zilivyovipunguza vya chini na vya katikati. 6 Maana vilikuwa vina orofa tatu, wala havikuwa na nguzo kama nguzo za zile nyua; basi kila kilichokuwa cha juu kilikuwa chembamba kuliko cha chini na cha katikati, kutoka chini. 7 Na ukuta ule uliokuwa nje, ubavuni mwa vyumba vile, ulioelekea ua wa nje, kuvikabili vyumba vile, urefu wake ni dhiraa hamsini. 8 Maana urefu wa vyumba vile, vilivyokuwa katika ua wa nje, ulikuwa dhiraa hamsini; na tazama, mbele ya hekalu, dhiraa mia. 9 Na toka chini ya vyumba vile palikuwa na mahali pa kuingilia upande wa mashariki, mtu aviingiavyo toka ua wa nje. 10 Tena palikuwa na vyumba katika unene wa ukuta wa ua, kuukabili upande wa mashariki, kupaelekea mahali palipotengeka, na kulielekea jengo. 11 Nayo njia iliyokuwa mbele yake, kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwake vyumba vile vilivyokuwa upande wa kaskazini, urefu ule ule, na upana ule ule; na mahali pake pa kutokea palikuwa sawasawa na vipimo vyake, na sawasawa na milango yake. 12 Na sawasawa na milango ya vyumba, vilivyoelekea upande wa kusini, palikuwa na mlango katika mwisho wa njia ile; yaani, njia iliyoukabili ukuta upande wa mashariki, mtu akiingia. 13 Kisha akaniambia, Vyumba vya upande wa kaskazini, na vyumba vya upande wa kusini, ambavyo vyaelekea mahali palipotengeka, ni vyumba vitakatifu; humo makuhani, wamkaribiao Bwana, watakula vitu vilivyo vitakatifu sana; humo wataviweka vitu vilivyo vitakatifu sana, na sadaka ya unga, na sadaka ya dhambi, na sadaka ya hatia; kwa maana mahali hapo ni patakatifu. 14 Makuhani watakapoingia ndani, hawatatoka mahali patakatifu kwenda hata ua wa nje; lakini wataweka mavazi yao katika mahali wahudumiapo; maana ni matakatifu; nao watavaa mavazi mengine, na kupakaribia mahali palipo mahali pa watu. 15 Basi, alipokuwa amekwisha kuipima nyumba ya ndani, akanileta nje, kwa njia ya lango lililokabili upande wa mashariki, akalipima pande zote. 16 Akaupima upande wa mashariki kwa mwanzi wa kupimia, mianzi mia tano, kwa mwanzi wa kupimia pande zote. 17 Akaupima upande wa kaskazini, mianzi mia tano, kwa mwanzi wa kupimia pande zote. 18 Akaupima upande wa kusini, mianzi mia tano, kwa mwanzi wa kupimia. 19 Akageuka aelekee upande wa magharibi, akapima mianzi mia tano, kwa mwanzi wa kupimia. 20 Alipima pande zake zote nne; lilikuwa na ukuta pande zote, urefu wake mianzi mia tano, na upana wake mianzi mia tano, ili kupatenga mahali palipo patakatifu, na mahali palipo pa watu wote.

Ezekieli 43

1 Kisha akanileta mpaka langoni, yaani, lango lile lielekealo upande wa mashariki; 2 na tazama, huo utukufu wa Mungu wa Israeli ulitokea kwa njia ya mashariki; na sauti yake ilikuwa kama mshindo wa maji mengi, nayo nchi iling'aa kwa utukufu wake. 3 Na maono niliyoyaona yalikuwa kama maono niliyoyaona nilipokuja kuuharibu mji; nayo maono niliyoyaona yalikuwa kama maono niliyoyaona karibu na mto wa Kebari; nikaanguka kifudifudi. 4 Na huo utukufu wa Bwana ukaingia ndani ya nyumba, kwa njia ya lango lile lielekealo upande wa mashariki. 5 Kisha Roho ikaniinua, ikanichukua mpaka ua wa ndani; na tazama, utukufu wa Bwana uliijaza nyumba. 6 Nikasikia sauti ya mmoja asemaye nami, itokayo katika nyumba hiyo; na mtu akasimama karibu nami. 7 Akaniambia, Mwanadamu, hapa ni mahali pa kiti changu cha enzi, na mahali pa nyayo za miguu yangu, nitakapokaa kati ya wana wa Israeli milele; na nyumba ya Israeli hawatalinajisi jina langu takatifu tena, wao, wala wafalme wao, kwa mambo yao ya kikahaba, na kwa mizoga ya wafalme wao, katika mahali pao pa juu; 8 kwa kuweka kizingiti chao karibu na kizingiti changu; na mwimo wao karibu na mwimo wangu; tena palikuwa na ukuta tu kati ya mimi na wao; nao wamelinajisi jina langu takatifu kwa machukizo yao waliyoyatenda; basi, kwa sababu hiyo, nimewakomesha katika hasira yangu. 9 Basi sasa wayaondoe mambo yao ya kikahaba, na mizoga ya wafalme wao, yawe mbali nami, nami nitakaa kati yao milele. 10 Na wewe, mwanadamu, waonyeshe wana wa Israeli nyumba hii, ili wayatahayarikie maovu yao; na waipime hesabu yake. 11 Na ikiwa wameyatahayarikia yote waliyoyatenda, waonyeshe umbo la nyumba, na namna yake, na matokeo yake, na maingilio yake, na maumbo yake yote, na maagizo yake yote, na kawaida zake zote, na sheria zake zote, ukayaandike machoni pao; ili walishike umbo lake lote, na maagizo yake, na kuyatenda. 12 Hii ndiyo sheria ya nyumba; juu ya kilele cha mlima, mpaka wake wote pande zote patakuwa patakatifu sana. Tazama, hii ndiyo sheria ya nyumba. 13 Na vipimo vya madhabahu kwa dhiraa ni hivi; (dhiraa ni dhiraa na shubiri); tako lake ni dhiraa moja, na upana wake dhiraa moja; na pambizo yake karibu na ncha yake pande zote, shubiri moja; na hili litakuwa tako la madhabahu. 14 Tena toka chini, juu ya nchi, hata daraja ya chini, dhiraa mbili, na upana wake dhiraa moja; tena toka daraja ndogo hata daraja kubwa, dhiraa nne, na upana wake dhiraa moja. 15 Na madhabahu ya juu itakuwa dhiraa nne; na toka madhabahu pawashwapo moto na kwenda juu zitakuwa pembe nne. 16 Na pale pawashwapo moto, urefu wake dhiraa kumi na mbili, na upana wake kumi na mbili, mraba pande zake nne. 17 Na daraja, urefu wake dhiraa kumi na nne, na upana wake dhiraa kumi na nne, pande zake nne; na pambizo yake nusu dhiraa; na tako lake dhiraa moja, kote kote, na madaraja yake yataelekea upande wa mashariki. 18 Kisha akaniambia, Mwanadamu, Bwana MUNGU asema hivi; Hizi ndizo sheria za madhabahu katika siku ile watakapoifanya, ili watoe sadaka za kuteketezwa juu yake, na kunyunyiza damu juu yake. 19 Utawapa makuhani Walawi, walio wa uzao wa Sadoki, walio karibu nami, ili kunihudumu, asema Bwana MUNGU, ng'ombe mume mchanga awe sadaka ya dhambi. 20 Nawe utatwaa baadhi ya damu yake, na kuitia juu ya pembe zake nne, na juu ya ncha nne za daraja, na juu ya pambizo yake pande zote; ndivyo utakavyoitakasa, na kuifanyia upatanisho. 21 Tena utamtwaa ng'ombe wa sadaka ya dhambi, naye utamteketeza mahali palipoamriwa pa nyumba ile, nje ya mahali patakatifu. 22 Na siku ya pili utamtoa beberu mkamilifu awe sadaka ya dhambi; nao wataisafisha madhabahu, kama walivyoisafisha kwa ng'ombe huyo. 23 Utakapokwisha kuitakasa, utatoa ng'ombe mume mchanga mkamilifu, na kondoo mume wa kundini mkamilifu. 24 Nawe utawaleta karibu mbele za Bwana, na makuhani watamwaga chumvi juu yao, nao watawatoa wawe sadaka za kuteketezwa kwa Bwana. 25 Kwa muda wa siku saba utaweka tayari mbuzi kila siku awe sadaka ya dhambi; pia wataweka tayari ng'ombe mume mchanga, na kondoo mume wa kundini, wakamilifu. 26 Kwa muda wa siku saba wataifanyia madhabahu upatanisho, na kuitakasa; ndivyo watakavyoiweka wakfu. 27 Nao watakapozitimiza siku hizo, itakuwa, siku ya nane na baadaye, makuhani watatoa sadaka zenu za kuteketezwa juu ya madhabahu, na sadaka zenu za amani nami nitawakubali ninyi, asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 44

1 Kisha akanirudisha kwa njia ya lango lile la nje, la mahali patakatifu lililoelekea upande wa mashariki; nalo lilikuwa limefungwa. 2 Bwana akaniambia, Lango hili litafungwa, halitafunguliwa, wala mtu awaye yote hataingia kwa lango hili, kwa maana Bwana, Mungu wa Israeli, ameingia kwa hilo; basi kwa sababu hiyo litafungwa. 3 Na mkuu, yeye ndiye atakayeketi ndani yake ale chakula mbele za Bwana; ataingia kwa njia ya ukumbi wa lango, naye atatoka kwa njia iyo hiyo. 4 Kisha akanileta, kwa njia ya lango la upande wa kaskazini, mbele ya nyumba; nikaangalia, na tazama, huo utukufu wa Bwana uliijaza nyumba ya Bwana; nikaanguka kifudifudi. 5 Bwana akaniambia, Mwanadamu, weka moyoni mwako, ukatazame kwa macho yako, ukasikie kwa masikio yako, maneno yote nitakayokuambia, katika habari ya kawaida zote za nyumba ya Bwana, na ya amri zake zote; nawe weka moyoni mwako maingilio ya nyumba, pamoja na matokeo yote ya mahali patakatifu. 6 Nawe utawaambia waasi, yaani nyumba ya Israeli, Bwana MUNGU asema hivi; Enyi nyumba ya Israeli, katika machukizo yenu yote, na iwatoshe, 7 kuwa mmewaingiza wageni, ambao mioyo yao haikutahiriwa, wala miili yao haikutahiriwa, wawe ndani ya patakatifu pangu, wapatie unajisi, naam, nyumba yangu, mtoapo sadaka ya chakula changu, mafuta na damu; nao wameyavunja maagano yangu, juu ya machukizo yenu yote. 8 Wala hamkuvilinda vitu vyangu vitakatifu bali mmejiwekea walinzi wa kawaida zangu, katika patakatifu pangu. 9 Bwana MUNGU asema hivi; Hapana mgeni, ambaye moyo wake haukutahiriwa, wala mwili wake haukutahiriwa, atakayeingia patakatifu pangu, miongoni mwa wageni walio kati ya wana wa Israeli. 10 Lakini Walawi waliofarakana nami, hapo Waisraeli walipopotea, waliopotea na kuvifuata vinyago vyao, watachukua uovu wao wenyewe. 11 Hata hivyo watakuwa wahudumu katika patakatifu pangu, wakiwa wasimamizi wa malango ya nyumba, wakihudumu humo nyumbani; watawachinjia watu sadaka za kuteketezwa na dhabihu, nao watasimama mbele yao ili kuwahudumia. 12 Kwa sababu waliwahudumia mbele ya vinyago vyao, wakawa kwazo la uovu kwa nyumba ya Israeli; basi nimeuinua mkono wangu juu yao, asema Bwana MUNGU, nao watachukua uovu wao. 13 Wala hawatanikaribia, kunihudumia katika kazi ya ukuhani, wala hawatakaribia vitu vyangu vitakatifu kimojawapo, vitu vilivyo vitakatifu sana; bali watachukua aibu yao, na machukizo yao yote waliyoyatenda. 14 Lakini nitawafanya kuwa walinzi katika ulinzi wa nyumba, kwa huduma yake yote, na kwa yote yatakayotendeka ndani yake. 15 Lakini makuhani Walawi, wana wa Sadoki, waliolinda ulinzi wa patakatifu pangu, hapo wana wa Israeli walipopotea na kuniacha, hao ndio watakaonikaribia ili kunihudumia; nao watasimama mbele zangu, kunitolea mafuta na damu, asema Bwana MUNGU; 16 wataingia patakatifu pangu, nao wataikaribia meza yangu, ili kunihudumia, nao watalinda ulinzi wangu. 17 Itakuwa, hapo watakapoingia kwa malango ya ua wa ndani, watavikwa mavazi ya kitani; wala sufu haitakuwa juu yao, maadamu wanahudumu katika malango ya ua wa ndani, na ndani ya nyumba. 18 Watakuwa na vilemba vya kitani juu ya vichwa vyao, nao watakuwa na suruali za kitani viunoni mwao; hawatajifunga kiunoni kitu cho chote kifanyacho jasho. 19 Nao watakapotoka kuingia ua wa nje, yaani, ua wa nje wa watu, ndipo watakapoyavua mavazi yao waliyovaa katika huduma yao, na kuyaweka katika vile vyumba vitakatifu, nao watavaa mavazi mengine, wasije wakawatakasa watu kwa mavazi yao. 20 Hawatanyoa vichwa vyao, wala hawataacha nywele zao kuwa ndefu sana; watazipunguza nywele za vichwa vyao tu. 21 Wala kuhani awaye yote hatakunywa mvinyo, aingiapo katika ua wa ndani. 22 Wala hawataoa wanawake wajane, wala mwanamke aliyeachwa na mume wake; lakini watatwaa mabikira wa wazao wa nyumba ya Israeli, au mjane aliyefiwa na mumewe kuhani. 23 Nao watawafundisha watu wangu tofauti iliyopo kati ya vitu vitakatifu na vitu vya sikuzote, na kuwafundisha kupambanua kati ya yaliyo machafu na yaliyo safi. 24 Na katika mashindano watasimama ili kuamua; wataamua sawasawa na hukumu zangu; nao watazishika sheria zangu, na amri zangu, katika sikukuu zangu zote zilizoamriwa; nao watazitakasa sabato zangu. 25 Wala hawatakaribia maiti na kujitia unajisi; ila kwa ajili ya baba, au mama, au mwana, au binti, au ndugu mwanamume, au ndugu mwanamke asiyeolewa bado, waweza kujitia unajisi. 26 Naye akiisha kutakaswa watamhesabia siku saba. 27 Na katika siku atakayoingia ndani ya patakatifu, katika ua wa ndani, ili kuhudumu ndani ya patakatifu, atatoa sadaka yake ya dhambi, asema Bwana MUNGU. 28 Nao watakuwa na urithi; mimi ni urithi wao; wala hamtawapa milki iwayo yote katika Israeli; mimi ni milki yao. 29 Wataila sadaka ya unga, na sadaka ya dhambi, na sadaka ya hatia, na kila kitu katika Israeli kilichowekwa wakfu kitakuwa chao. 30 Na kitu cha kwanza cha malimbuko yote ya vitu vyote, na kila toleo la kila kitu cha matoleo yenu, litakuwa la makuhani. Tena mtampa kuhani sehemu ya kwanza ya unga mbichi, ili kukalisha baraka juu ya nyumba yako. 31 Makuhani hawatakula nyamafu, au iliyoraruliwa, ikiwa ya ndege au ya mnyama.

Ezekieli 45

1 Tena, mtakapoigawanya nchi kwa kura iwe urithi, mtamtolea Bwana toleo, sehemu takatifu ya nchi, urefu wake utakuwa urefu wa mianzi ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi; itakuwa takatifu ndani ya mipaka yake yote pande zote. 2 Katika hiyo itakuwako sehemu kwa mahali patakatifu, urefu wake mia tano, na upana wake mia tano, mraba pande zote; na dhiraa ishirini kwa viunga vyake pande zote. 3 Na kwa kipimo hicho utapima, urefu wa ishirini na tano elfu, na upana wa elfu kumi; na ndani yake patakuwa patakatifu, palipo patakatifu sana. 4 Hiyo ni sehemu takatifu ya nchi; itakuwa ya makuhani, wahudumu wa patakatifu, wakaribiao kumhudumia Bwana; nayo itakuwa mahali kwa nyumba zao, na patakatifu kwa mahali patakatifu. 5 Tena urefu wa ishirini na tano elfu, na upana wa elfu kumi, ni sehemu ya Walawi, wahudumu wa nyumba, iwe milki yao wenyewe kwa vyumba ishirini. 6 Nanyi mtaiandika milki ya mji, upana wake elfu tano, na urefu wake ishirini na tano elfu, kandokando ya mahali palipotolewa, iwe sehemu takatifu; nayo itakuwa ya nyumba yote ya Israeli. 7 Na sehemu itakayokuwa ya mkuu itakuwa upande huu, na upande huu, wa toleo takatifu, na wa milki ya mji, kulikabili toleo takatifu, na kuikabili milki ya mji, upande wa magharibi kuelekea magharibi, na upande wa mashariki kuelekea mashariki; na kwa urefu wake sawasawa na sehemu mojawapo, toka mpaka wa magharibi hata mpaka wa mashariki. 8 Katika nchi hiyo itakuwa milki kwake katika Israeli; wala wakuu wangu hawatawaonea watu wangu tena kabisa; bali watawapa nyumba ya Israeli nchi hiyo, kwa kadiri ya makabila yao. 9 Bwana MUNGU asema hivi; Na iwatoshe ninyi, enyi wakuu wa Israeli; ondoeni dhuluma na unyang'anyi; fanyeni hukumu na haki; ondoeni kutoza kwa nguvu kwenu katika watu wangu, asema Bwana MUNGU. 10 Mtakuwa na mizani ya haki, na efa ya haki, na bathi ya haki. 11 Efa na bathi zitakuwa za kipimo kimoja; ili kwamba bathi ichukue sehemu ya kumi ya homeri, na efa sehemu ya kumi ya homeri; kipimo chake kitakuwa kwa kadiri ya cheo cha kawaida cha homeri. 12 Nayo shekeli itakuwa gera ishirini; shekeli tano zitakuwa shekeli tano, shekeli kumi zitakuwa kumi, na shekeli hamsini zitakuwa mane yenu. 13 Toleo mtakalotoa ni hili; sehemu ya sita ya efa katika homeri moja ya ngano, nanyi mtatoa sehemu ya sita ya efa katika homeri ya shayiri; 14 na sehemu ya mafuta iliyoamriwa, katika bathi ya mafuta, itakuwa sehemu ya kumi ya bathi katika kori moja, ambayo ni bathi kumi, yaani homeri; maana bathi kumi ni homeri moja; 15 na mwana-kondoo mmoja wa kundi katika mia mbili, katika malisho ya Israeli yenye maji; kwa sadaka ya unga, na kwa sadaka ya kuteketezwa, na kwa sadaka za amani, ili kuwafanyia upatanisho, asema Bwana MUNGU. 16 Watu wote wa nchi watatoa toleo hili kwa ajili ya mkuu katika Israeli. 17 Tena itakuwa kazi ya mkuu kutoa hizo sadaka za kuteketezwa, na sadaka za unga, na sadaka za vinywaji, katika sikukuu, na katika mwezi mpya, na katika sabato, katika sikukuu zote za nyumba ya Israeli zilizoamriwa; atatengeneza sadaka ya dhambi, na sadaka ya unga, na sadaka ya kuteketezwa, na sadaka za amani, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nyumba ya Israeli. 18 Bwana MUNGU asema hivi; Mwezi wa kwanza, siku ya kwanza ya mwezi, utatwaa ng'ombe mchanga mume mkamilifu; nawe utapatakasa mahali patakatifu. 19 Na kuhani atatwaa baadhi ya damu ya sadaka ya dhambi, na kuitia juu ya miimo ya milango ya nyumba, na juu ya pembe nne za daraja ya madhabahu, na juu ya miimo ya lango la ua wa ndani. 20 Nawe utafanya vivyo hivyo katika mwezi wa saba, siku ya kwanza ya mwezi kwa ajili ya kila mtu akosaye, na kwa ajili ya mtu aliye mjinga, ndivyo mtakavyoifanyia nyumba upatanisho. 21 Mwezi wa kwanza, siku ya kumi na nne ya mwezi, mtakuwa na Pasaka, sikukuu ya siku saba; mkate usiotiwa chachu utaliwa. 22 Na siku hiyo mkuu atatengeneza ng'ombe kuwa sadaka ya dhambi, kwa ajili ya nafsi yake, na kwa ajili ya watu wote wa nchi. 23 Tena, katika zile siku saba za sikukuu atamtengenezea Bwana sadaka ya kuteketezwa, ng'ombe saba na kondoo waume saba wakamilifu, kila siku kwa muda wa siku saba, na beberu mmoja kila siku kuwa sadaka ya dhambi. 24 Naye atatengeneza sadaka ya unga, efa moja kwa ng'ombe, na efa moja kwa kondoo mume, na hini moja ya mafuta kwa efa moja; 25 katika mwezi wa saba, siku ya kumi na tano ya mwezi, katika sikukuu atafanya vivyo hivyo kwa muda wa siku saba; sadaka ya dhambi vivyo hivyo, na sadaka ya kuteketezwa vivyo hivyo, na sadaka ya unga vivyo hivyo, na mafuta vivyo hivyo.

Ezekieli 46

1 Bwana MUNGU asema hivi; Lango la ua wa ndani, lielekealo upande wa mashariki litafungwa siku sita za kazi; lakini siku ya sabato litafunguliwa, na siku ya mwezi mpya litafunguliwa. 2 Naye mkuu ataingia kwa njia ya ukumbi wa lango lile, upande wa nje, naye atasimama karibu na mwimo wa lango, nao makuhani wataitengeneza sadaka yake ya kuteketezwa, na sadaka zake za amani, naye ataabudu penye kizingiti cha lango; kisha atatoka; lakini lango lile halitafungwa hata wakati wa jioni. 3 Watu wa nchi nao wataabudu mbele ya mlango wa lile lango mbele za Bwana, siku za sabato, na siku za mwezi mpya. 4 Nayo sadaka ya kuteketezwa, ambayo mkuu atamtolea Bwana siku ya sabato, itakuwa wana-kondoo sita wakamilifu, na kondoo mume mkamilifu. 5 Na sadaka ya unga itakuwa efa moja kwa kondoo mume, na sadaka ya unga kwa wale wana-kondoo, kiasi awezacho kutoa, na hini moja ya mafuta kwa efa moja. 6 Na siku ya mwezi mpya itakuwa ni ng'ombe mume mchanga mkamilifu; na wana-kondoo sita, na kondoo mume; nao watakuwa wakamilifu. 7 Naye atatengeneza sadaka ya unga, efa moja kwa ng'ombe mume, na efa moja kwa kondoo mume, na kwa wale wana-kondoo, kwa kiasi awezacho kutoa, na hini moja ya mafuta kwa efa moja. 8 Naye mkuu atakapoingia, ataingia kwa njia ya ukumbi wa lango lile, naye atatoka kwa njia iyo hiyo. 9 Lakini watu wa nchi watakapokuja mbele za Bwana katika sikukuu zilizoamriwa, yeye aingiaye kwa njia ya lango la upande wa kaskazini ili kuabudu, atatoka kwa njia ya lango la upande wa kusini; na yeye aingiaye kwa njia ya lango la upande wa kusini, atatoka kwa njia ya lango la upande wa kaskazini; hatarudi kwa njia ya lango aliloingia kwalo, lakini atatoka kwa kwenda mbele moja kwa moja. 10 Naye mkuu atakapoingia, ataingia katikati yao, nao, watakapotoka, watatoka wote pamoja. 11 Na katika sikukuu hizo, na sikukuu nyingine zilizoamriwa, sadaka ya unga itakuwa efa moja kwa ng'ombe mmoja, na efa moja kwa kondoo mume mmoja, na kwa wale wana-kondoo kiasi awezacho kutoa, na hini moja ya mafuta kwa efa moja. 12 Naye mkuu atakapotengeneza sadaka atoayo kwa hiari yake mwenyewe, sadaka ya kuteketezwa, au sadaka za amani, ziwe sadaka amtoleazo Bwana kwa hiari yake mwenyewe, mtu mmoja atamfungulia lango lile lielekealo upande wa mashariki, naye ataitengeneza sadaka yake ya kuteketezwa, na sadaka zake za amani, kama afanyavyo siku ya sabato; kisha atatoka; na baada ya kutoka kwake mtu mmoja atalifunga lango. 13 Nawe utatengeneza mwana-kondoo wa mwaka wa kwanza, mkamilifu, kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Bwana kila siku; kila siku asubuhi utamtengeneza. 14 Nawe utatengeneza sadaka ya unga pamoja nayo kila siku asubuhi, sehemu ya sita ya efa moja, na sehemu ya tatu ya hini moja ya mafuta; kuchanganya na unga ule mzuri; sadaka ya unga kwa Bwana daima, kwa amri ya milele. 15 Hivyo ndivyo watakavyomtengeneza mwana-kondoo, na sadaka ya unga, na mafuta, kila siku asubuhi, kuwa sadaka ya kuteketezwa ya daima. 16 Bwana MUNGU asema hivi; Mkuu akimpa mwanawe awaye yote zawadi, ni urithi wake, itakuwa mali ya wanawe; ni milki yao kwa kurithiwa. 17 Bali akimpa mmoja wa watumishi wake baadhi ya urithi wake, itakuwa mali yake mpaka mwaka wa kuacha huru; ndipo itakapomrudia mkuu; lakini urithi wake, huo utakuwa wa wanawe. 18 Tena mkuu hatawaondolea watu urithi wao, hata kuwatoa kwa nguvu katika milki yao; atawapa wanawe urithi katika mali yake mwenyewe, watu wangu wasije wakatawanyika, kila mtu mbali na milki yake. 19 Ndipo akanileta kati ya maingilio, yaliyokuwa kando ya lango, mpaka vyumba vitakatifu vya makuhani, vilivyoelekea upande wa kaskazini; na tazama, palikuwa na mahali, upande wa nyuma ulioelekea magharibi. 20 Akaniambia, Hapa ndipo mahali pa makuhani, watakapoitokosa sadaka ya hatia, na sadaka ya dhambi, watakapoioka sadaka ya unga; kusudi wasizilete nje katika ua wa nje, na kuwatakasa watu. 21 Kisha akanileta mpaka ua wa nje, akanipitisha karibu na pembe nne za ua huo; na tazama, katika kila pembe ya ua huo palikuwa na kiwanja. 22 Katika pembe nne za ua huo palikuwa na viwanja vilivyoungana, urefu wake dhiraa arobaini, na upana wake thelathini; viwanja hivyo vinne vya pembeni vilikuwa vya kipimo kimoja. 23 Tena palikuwa na safu ndani yake pande zote, kuvizunguka vile viwanja vinne; tena palifanywa meko ya kutokosea, chini ya safu pande zote. 24 Ndipo akaniambia, Hizi ni nyumba za kutokosea, ambamo wahudumu wa nyumba watatokosa sadaka za watu.

Ezekieli 47

1 Baadaye akanileta tena mpaka lango la nyumba; na tazama, maji yalitoka chini ya kizingiti cha nyumba, kwa njia ya mashariki, maana upande wa mbele wa nyumba ulielekea upande wa mashariki; nayo maji yakashuka toka chini ya upande wa kuume wa nyumba, upande wa kusini wa madhabahu. 2 Ndipo akanileta nje kwa njia ya lango upande wa kaskazini, akanizungusha kwa njia ya nje mpaka lango la nje, kwa njia yake iliyoelekea mashariki; na tazama, maji yalitoka upande wa kuume. 3 Na alipotoka mtu yule, mwenye uzi wa kupimia mkononi mwake, kwenda masharikini, akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale; maji yakafika mpaka viweko vya miguu. 4 Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale, maji yakafika mpaka magoti. Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha, maji yakafika mpaka viuno. 5 Kisha akapima dhiraa elfu, yakawa mto nisioweza kuuvuka; maana maji yamezidi, maji ya kuogelea, mto usiovukika. 6 Akaniambia, Mwanadamu, je! Umeona haya? Kisha akanichukua akanirudisha mpaka ukingo wa mto. 7 Basi nikiisha kurudi, tazama, kando ya ukingo wa mto ilikuwapo miti mingi sana, upande huu na upande huu. 8 Ndipo akaniambia, Maji haya yanatoka kwenda pande za nchi ya mashariki, nayo yanashuka mpaka Araba, na kuingia katika bahari maji yatokezwayo yataingia baharini ,na maji yake yataponyeka. 9 Tena itakuwa, kila kiumbe hai kisongamanacho, kila mahali itakapofika mito hiyo, kitaishi; kutakuwapo wingi mkubwa wa samaki, kwa sababu maji haya yamefika huko maana maji yale yataponyeka, na kila kitu kitaishi po pote utakapofikilia mto huo. 10 Tena itakuwa, wavuvi watasimama karibu nao; toka Engedi mpaka En-eglaimu, patakuwa ni mahali pa kutandazia nyavu; samaki wao watakuwa namna zao mbalimbali, kama samaki wa bahari kubwa, wengi sana. 11 Bali mahali penye matope, na maziwa yake, hayataponywa; yataachwa yawe ya chumvi. 12 Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula, ambao majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; utatoa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu; na matunda yake yatakuwa ni chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa. 13 Bwana MUNGU asema hivi; Huu ndio mpaka ambao mtaigawanya nchi iwe urithi sawasawa na kabila kumi na mbili za Israeli; kwa Yusufu, mafungu mawili. 14 Nanyi mtaimiliki, mtu huyu sawasawa na huyu; ambayo naliuinua mkono wangu kuwapa baba zenu; na nchi hii itawaangukia kuwa urithi. 15 Na huu ndio mpaka wa nchi; upande wa kaskazini, toka bahari kubwa, kwa njia ya Hethloni, mpaka maingilio ya Sedada; 16 Hamathi, na Berotha, na Sibraimu, ulio katikati ya mpaka wa Dameski na mpaka wa Hamathi; na Haser-hatikoni, ulio karibu na mpaka wa Haurani. 17 Nao mpaka toka baharini utakuwa Hasar-enoni, penye mpaka wa Dameski, na kaskazini kuelekea upande wa kaskazini ndio mpaka wa Hamathi. Huu ndio upande wa kaskazini. 18 Na upande wa mashariki, kati ya Haurani na Dameski, na Gileadi na nchi ya Israeli, utakuwa mto Yordani; mtapima toka mpaka wa upande wa kaskazini hata bahari ya mashariki. Huu ndio upande wa mashariki. 19 Na upande wa kusini, kuelekea kusini, utakuwa ni kutoka Tamari mpaka maji ya Meriba-Kadeshi, mpaka kijito cha Misri, mpaka bahari kubwa. Huu ndio upande wa kusini, kuelekea kusini. 20 Na upande wa magharibi, utakuwa ni bahari kubwa, kutoka mpaka wa kusini mpaka mahali penye kuelekea maingilio ya Hamathi. Huu ndio upande wa magharibi. 21 Basi ndivyo mtakavyojigawanyia nafsi zenu nchi hii, sawasawa na kabila za Israeli. 22 Tena itakuwa mtaigawanya kwa kura, kuwa urithi kwenu, na kwa wageni wakaao kwenu hali ya ugeni, watakaozaa watoto kati yenu, nao watakuwa kwenu, kama wazaliwa miongoni mwa wana Israeli; watakuwa na urithi pamoja nanyi kati ya kabila za Israeli. 23 Tena itakuwa, mgeni akaaye katika kabila iwayo yote, atapewa urithi katika kabila asema Bwana MUNGU.

Ezekieli 48

1 Basi, haya ndiyo majina ya kabila hizo; toka mwisho wa pande za kaskazini, karibu na njia ya Hethloni, hata maingilio ya Hamathi, hata Hasar-enoni, penye mpaka wa Dameski, yaani, upande wa kaskazini karibu na Hamathi, watakuwa na upande wa mashariki, na upande wa magharibi; Dani fungu moja. 2 Tena mpakani mwake Dani, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Asheri, fungu moja. 3 Na mpakani mwa Asheri, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Naftali, fungu moja. 4 Na mpakani mwa Naftali, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Manase, fungu moja. 5 Na mpakani mwa Manase, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Efraimu, fungu moja. 6 Na mpakani mwa Efraimu, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Reubeni, fungu moja. 7 Na mpakani mwa Reubeni, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Yuda, fungu moja. 8 Na mpakani mwa Yuda, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi, yatakuwapo matoleo mtakayotoa, upana wake mianzi ishirini na tano elfu, na urefu wake sawasawa na moja la mafungu hayo, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; na mahali patakatifu ni katikati yake. 9 Matoleo hayo, mtakayomtolea Bwana, urefu wake ni mianzi ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi. 10 Matoleo hayo matakatifu yatakuwa kwa watu hawa, kwa makuhani; upande wa kaskazini urefu wake ishirini na tano elfu, na upande wa magharibi upana wake elfu kumi, na upande wa mashariki upana wake elfu kumi, na upande wa kusini urefu wake ishirini na tano elfu; na mahali patakatifu pa Bwana patakuwa katikati yake. 11 Patakuwa kwa makuhani wa wana wa Sadoki, waliotakasika, walioulinda ulinzi wangu, wasioasi, wana wa Israeli walipoasi, kama Walawi walivyoasi. 12 Na matoleo hayo ya nchi yatolewayo, yatakuwa kwao kitu kitakatifu sana, karibu na mpaka wa Walawi. 13 Na kuukabili mpaka wa makuhani, Walawi watakuwa na fungu, urefu wake ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi; urefu wote utakuwa ishirini na tano elfu, na upana wake elfu kumi. 14 Wala hawatauza sehemu yake, wala kuibadili, wala hawatawapa wengine malimbuko ya nchi; maana ni matakatifu kwa Bwana. 15 Na mianzi elfu tano iliyosalia katika upana, kuikabili hiyo ishirini na tano elfu, itatumiwa na watu wote, kwa huo mji, na kwa maskani, na kwa viunga, na huo mji utakuwa katikati yake. 16 Na vipimo vyake ni hivi; upande wa kaskazini elfu nne na mia tano, na upande wa kusini elfu nne na mia tano, na upande wa mashariki elfu nne na mia tano, na upande wa magharibi elfu nne na mia tano. 17 Nao mji utakuwa na malisho; upande wa kaskazini mia mbili na hamsini, na upande wa kusini mia mbili na hamsini, na upande wa mashariki mia mbili na hamsini, na upande wa magharibi mia mbili na hamsini. 18 Na mabaki ya urefu wake yaelekeayo matoleo matakatifu, upande wa mashariki yatakuwa elfu kumi, na upande wa magharibi elfu kumi; nayo yatakuwa sawasawa na matoleo matakatifu; na mazao yake yatakuwa ni chakula cha watu wafanyao kazi humo mjini. 19 Na hao wafanyao kazi mjini, wa kabila zote za Israeli, watailima nchi hiyo. 20 Matoleo yote yatakuwa ishirini na tano elfu, kwa ishirini na tano elfu; mtatoa matoleo matakatifu, nchi ya mraba, pamoja na milki ya mji. 21 Nayo mabaki yake yatakuwa ya huyo mkuu, upande huu na upande huu wa matoleo matakatifu, na milki ya mji, kuikabili hiyo ishirini na tano elfu ya matoleo, kuelekea mpaka wa mashariki; tena upande wa magharibi kuikabili hiyo ishirini na tano elfu, upande wa kuelekea mpaka wa magharibi; sawa na yale mafungu, hayo yatakuwa ya huyo mkuu; na matoleo matakatifu na mahali patakatifu pa nyumba patakuwa katikati yake. 22 Tena tokea milki ya Walawi, na tokea milki ya mji, kwa kuwa ni katikati ya nchi iliyo ya mkuu, katikati ya mpaka wa Yuda na mpaka wa Benyamini, itakuwa ya mkuu. 23 Na katika habari za kabila zilizosalia; toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Benyamini, fungu moja. 24 Tena mpakani mwa Benyamini, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Simeoni, fungu moja. 25 Tena mpakani mwa Simeoni, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Isakari, fungu moja. 26 Na mpakani mwa Isakari, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Zabuloni, fungu moja. 27 Na mpakani mwa Zabuloni, toka upande wa mashariki hata upande wa magharibi; Gadi, fungu moja. 28 Na mpakani mwa Gadi, upande wa kusini kuelekea kusini, mpaka wake utakuwa toka Tamari, mpaka maji ya Meriba-Kadeshi, mpaka kijito cha Misri, mpaka bahari kubwa. 29 Hiyo ndiyo nchi mtakayozigawanyia kabila za Israeli, kuwa urithi wao, na hayo ndiyo mafungu yao, asema Bwana MUNGU. 30 Na matokeo ya mji ndiyo haya; upande wa kaskazini, mianzi elfu nne na mia tano, kwa kupima; 31 na malango ya mji yatatajwa kwa majina ya kabila za Israeli, malango matatu upande wa kaskazini; lango la Reubeni, moja; lango la Yuda, moja; na lango la Lawi, moja. 32 Na upande wa mashariki, elfu nne na mia tano, kwa kupima; na malango matatu; lango la Yusufu, moja; lango la Benyamini, moja; lango la Dani, moja. 33 Na upande wa kusini, elfu nne na mia tano kwa kupima; na malango matatu; lango la Simeoni, moja; lango la Isakari, moja; lango la Zabuloni, moja. 34 Na upande wa magharibi, elfu nne na mia tano; pamoja na malango yake matatu; lango la Gadi, moja; lango la Asheri, moja; na lango la Naftali, moja. 35 Kuuzunguka ni mianzi kumi na nane elfu; na jina la mji huo tangu siku hiyo litakuwa hili, Bwana yupo hapa.

Danieli 1

1 Katika mwaka wa tatu wa kumiliki kwake Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, Nebukadreza mfalme wa Babeli,alikwenda Yerusalemu akauhusuru. 2 Bwana akamtia Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, katika mkono wake, pamoja na baadhi ya vyombo vya nyumba ya Mungu; naye akavichukua mpaka nchi ya Shinari, mpaka nyumba ya mungu wake; akaviingiza vile vyombo katika nyumba ya hazina ya mungu wake. 3 Mfalme akamwambia Ashpenazi, mkuu wa matowashi wake, awalete baadhi ya wana wa Israeli, wa uzao wa kifalme, na wa uzao wa kiungwana; 4 vijana wasio na mawaa, wazuri wa uso, wajuzi wa hekima, werevu kwa sababu ya maarifa yao, wenye kufahamu elimu, watakaoweza kusimama katika jumba la mfalme; tena alimwambia awafundishe elimu ya Wakaldayo, na lugha yao. 5 Huyo mfalme akawaagizia posho ya chakula cha mfalme, na ya divai aliyokunywa, akaagiza walishwe hivyo muda wa miaka mitatu; ili kwamba hatimaye wasimame mbele ya mfalme. 6 Basi katika hao walikuwapo baadhi ya wana wa Yuda, Danielii, na Hanania, na Mishaeli, na Azaria. 7 Mkuu wa matowashi akawapa majina; alimwita Danielii, Belteshaza; na Hanania akamwita Shadraka; na Mishaeli akamwita Meshaki; na Azaria akamwita Abednego. 8 Lakini Danielii aliazimu moyoni mwake ya kuwa hatajitia unajisi kwa chakula cha mfalme, wala kwa divai aliyokunywa; basi akamwomba yule mkuu wa matowashi ampe ruhusa asijitie unajisi. 9 Basi Mungu alimjalia Danielii kupata kibali na huruma machoni pa huyo mkuu wa matowashi. 10 Mkuu wa matowashi akamwambia Danielii, Mimi namwogopa bwana wangu, mfalme, aliyewaagizia ninyi chakula chenu na kinywaji chenu; kwa nini azione nyuso zenu kuwa hazipendezi kama nyuso za vijana hirimu zenu? Basi kwa kufanya hivyo mtahatirisha kichwa changu mbele ya mfalme. 11 Ndipo Danielii akamwambia yule msimamizi, ambaye mkuu wa matowashi amemweka juu ya Danielii, na Hanania, na Mishaeli, na Azaria, 12 Tafadhali utujaribu sisi watumishi wako muda wa siku kumi; na watupe mtama tule, na maji tunywe. 13 Kisha nyuso zetu zitazamwe mbele yako, na nyuso za wale vijana wanaokula chakula cha mfalme; ukatutendee sisi watumishi wako kadiri ya utakavyoona. 14 Basi akawasikiliza katika jambo hilo, akawajaribu siku kumi. 15 Hata mwisho wa zile siku kumi nyuso zao zilikuwa nzuri zaidi, na miili yao ilikuwa imenenepa zaidi, kuliko wale vijana wote waliokula chakula cha mfalme. 16 Basi yule msimamizi akaiondoa posho yao ya chakula, na ile divai waliyopewa wanywe, akawapa mtama tu. 17 Basi, kwa habari za hao vijana wanne, Mungu aliwapa maarifa na ujuzi katika elimu na hekima; Danielii naye alikuwa na ufahamu katika maono yote, na ndoto. 18 Hata mwisho wa siku zile alizoziagiza mfalme za kuwaingiza, mkuu wa matowashi akawaingiza mbele ya mfalme Nebukadreza. 19 Naye mfalme akazungumza nao; na miongoni mwao wote hawakuonekana waliokuwa kama Danielii, na Hanania, na Mishaeli, na Azaria; kwa hiyo wakasimama mbele ya mfalme. 20 Na katika kila jambo la hekima na ufahamu alilowauliza mfalme, akawaona kuwa walifaa mara kumi zaidi ya waganga na wachawi waliokuwa katika ufalme wake. 21 Tena, Danielii huyo akadumu huko hata mwaka wa kwanza wa mfalme Koreshi.

Danieli 2

1 Hata katika mwaka wa pili wa kumiliki kwake Nebukadreza, Nebukadreza aliota ndoto; na roho yake ikafadhaika, usingizi wake ukamwacha. 2 Ndipo mfalme akatoa amri kuwaita waganga, na wachawi, na wasihiri, na Wakaldayo, wapate kumweleza mfalme ndoto zake. Basi wakaingia, wakasimama mbele ya mfalme. 3 Mfalme akawaambia, Nimeota ndoto, na roho yangu imefadhaika hata niijue tafsiri yake. 4 Ndipo hao Wakaldayo wakamwambia mfalme, kwa lugha ya Kiaramu, Ee Mfalme, uishi milele; tuambie sisi watumishi wako ile ndoto, nasi tutakuonyesha tafsiri yake. 5 Mfalme akajibu, akawaambia Wakaldayo, Neno lenyewe limeniondoka; msiponijulisha ile ndoto na tafsiri yake, mtakatwa vipande vipande, na nyumba zenu zitafanywa jaa. 6 Bali kama mkinionyesha ile ndoto na tafsiri yake, nitawapa zawadi na thawabu na heshima nyingi; basi nionyesheni ile ndoto na tafsiri yake. 7 Wakajibu mara ya pili, wakasema, Mfalme na atuambie sisi watumishi wake ile ndoto, nasi tutamwonyesha tafsiri yake. 8 Mfalme akajibu, akasema, Najua hakika ya kuwa mnataka kupata nafasi, kwa sababu mmeona ya kuwa lile neno lenyewe limeniondoka. 9 Lakini msiponijulisha ile ndoto, iko amri moja tu iwapasayo; maana mmepatana kusema maneno ya uongo, na maneno maovu, mbele yangu, hata zamani zitakapobadilika; basi niambieni ile ndoto, nami nitajua ya kuwa mwaweza kunionyesha tafsiri yake. 10 Wakaldayo wakajibu mbele ya mfalme, wakasema, Hapana mtu duniani awezaye kulionyesha neno hili la mfalme; kwa maana hapana mfalme, wala bwana, wala liwali, aliyetaka neno kama hili kwa mganga, wala kwa mchawi, wala kwa Mkaldayo. 11 Ni neno la ajabu, hili analolitaka mfalme, wala hapana mwingine awezaye kumwonyesha mfalme neno hilo, ila miungu, wasio na kikao pamoja na wenye mwili. 12 Basi kwa hiyo mfalme akaghadhibika sana, akaona hasira nyingi, akatoa amri kuwaangamiza wenye hekima wote wa Babeli. 13 Basi ile amri ikatangazwa, na hao wenye hekima walikuwa karibu na kuuawa; watu wakamtafuta Danielii na wenzake ili wauawe. 14 Ndipo Danielii kwa busara na hadhari akamjibu Arioko, akida wa walinzi wa mfalme, aliyekuwa ametoka ili kuwaua wenye hekima wa Babeli; 15 alijibu, akamwambia Arioko, akida wa walinzi wa mfalme, Mbona amri hii ya mfalme ina ukali namna hii? Ndipo Arioko akamwarifu Danielii habari ile. 16 Basi Danielii akaingia, akamwomba mfalme ampe muda, kisha yeye atamwonyesha mfalme tafsiri ile. 17 Ndipo Danielii akaenda nyumbani kwake, akawapasha habari kina Hanania, na Mishaeli, na Azaria wenzake; 18 ili waombe rehema kwa Mungu wa mbinguni kwa habari ya siri hiyo, ili kwamba Danielii na wenzake wasiangamizwe pamoja na wenye hekima wa Babeli. 19 Ndipo Danielii alipofunuliwa siri hiyo katika njozi ya usiku. Basi Danielii akamhimidi Mungu wa mbinguni. 20 Danielii akajibu, akasema, Na lihimidiwe jina la Mungu milele na milele; kwa kuwa hekima na uweza ni wake. 21 Yeye hubadili majira na nyakati; huuzulu wafalme na kuwamilikisha wafalme; huwapa hekima wenye hekima; huwapa wenye ufahamu maarifa; 22 yeye hufunua mambo ya fumbo na ya siri; huyajua yaliyo gizani, na nuru hukaa kwake. 23 Nakushukuru, nakuhimidi, Ee Mungu wa baba zangu, uliyenipa hekima na uwezo, ukanijulisha hayo tuliyotaka kwako; maana umetujulisha neno lile la mfalme. 24 Basi Danielii akaenda kwa Arioko, aliyewekwa na mfalme kuwaangamiza wenye hekima wa Babeli; alikwenda akamwambia hivi, Usiwaangamize wenye hekima wa Babeli; niingize mimi mbele ya mfalme, nami nitamwonyesha mfalme ile tafsiri. 25 Ndipo Arioko akamwingiza Danielii mbele ya mfalme kwa haraka, akamwambia hivi, Nimemwona mtu wa hao wana wa Yuda waliohamishwa, atakayemjulisha mfalme ile tafsiri. 26 Mfalme akajibu, akamwambia Danielii, aliyekuwa akiitwa Belteshaza, Je! Waweza kunijulisha ile ndoto niliyoiona, na tafsiri yake. 27 Danielii akajibu mbele ya mfalme, akasema, Ile siri aliyoiuliza mfalme, wenye hekima hawawezi kumfunulia mfalme; wala wachawi, wala waganga, wala wanajimu; 28 lakini yuko Mungu mbinguni afunuaye siri, naye amemjulisha mfalme Nebukadreza mambo yatakayokuwa siku za mwisho. Ndoto yako, na njozi za kichwa chako ulizoziona kitandani pako, ni hizi; 29 Wewe, Ee mfalme, mawazo yako yaliingia moyoni mwako kitandani pako ya mambo yatakayokuwa halafu; na yeye afunuaye siri amekujulisha mambo yatakayokuwa. 30 Lakini mimi, sikufunuliwa siri hii kwa sababu ya hekima iwayo yote niliyo nayo zaidi ya watu wengine walio hai, bali kusudi mfalme afunuliwe ile tafsiri, nawe upate kujua mawazo ya moyo wako. 31 Wewe, Ee Mfalme, uliona, na tazama, sanamu kubwa sana. Sanamu hii, iliyokuwa kubwa sana, na mwangaza wake mwingi sana, ilisimama mbele yako; na umbo lake lilikuwa lenye kutisha. 32 Na sanamu hii kichwa chake kilikuwa ni cha dhahabu safi; kifua chake na mikono yake ni ya fedha; tumbo lake na viuno vyake ni vya shaba; 33 miguu yake ni ya chuma; na nyayo za miguu yake nusu ya chuma na nusu ya udongo. 34 Nawe ukatazama hata jiwe likachongwa bila kazi ya mikono, nalo jiwe hilo likaipiga sanamu miguu yake, iliyokuwa ya chuma na udongo, likaivunja vipande vipande. 35 Ndipo kile chuma, na ule udongo, na ile shaba, na ile fedha, na ile dhahabu, vilivunjwa vipande vipande pamoja vikawa kama makapi ya viwanja vya kupepetea wakati wa hari; upepo ukavipeperusha hata pasionekane mahali pake; na lile jiwe lililoipiga hiyo sanamu likawa milima mikubwa, likaijaza dunia yote. 36 Hii ndiyo ile ndoto, nasi tutaihubiri tafsiri yake mbele ya mfalme. 37 Wewe, Ee mfalme, u mfalme wa wafalme, na Mungu wa mbinguni amekupa ufalme, na uwezo, na nguvu, na utukufu; 38 na kila mahali wakaapo wanadamu, wanyama wa kondeni na ndege wa angani amewatia mkononi mwako, naye amekumilikisha juu ya hao wote; wewe u kichwa kile cha dhahabu. 39 Na baada ya zamani zako utainuka ufalme mwingine mdogo kuliko wewe; na ufalme mwingine wa tatu wa shaba, utakaoitawala dunia yote. 40 Na ufalme wa nne utakuwa na nguvu mfano wa chuma; kwa maana chuma huvunja vitu vyote na kuvishinda; na kama chuma kisetavyo vitu hivi vyote, ndivyo utakavyovunja-vunja na kuseta. 41 Na kama vile ulivyoziona hizo nyayo za miguu na vidole vyake, kuwa nusu udongo wa mfinyanzi, na nusu chuma, ufalme ule utakuwa ufalme uliogawanyika; lakini ndani yake zitakuwako nguvu za chuma, kama vile ulivyoona kile chuma kimechanganyika na udongo wa matope. 42 Na kama vidole vya zile nyayo vilikuwa nusu chuma na nusu udongo, kadhalika ufalme ule utakuwa nusu yake una nguvu, na nusu yake umevunjika. 43 Na kama vile ulivyokiona kile chuma kimechanganyika na udongo wa matope, watajichanganya nafsi zao kwa mbegu za wanadamu; lakini hawatashikamana, kama vile chuma kisivyoshikamana na udongo. 44 Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele. 45 Na kama vile ulivyoona ya kuwa jiwe lilichongwa mlimani bila kazi ya mikono, na ya kuwa lilivunja-vunja kile chuma, na ile shaba na ule udongo, na ile fedha, na ile dhahabu; basi Mungu aliye mkuu amemjulisha mfalme mambo yatakayokuwa baadaye; na ndoto hii ni ya hakika, na tafsiri yake ni thabiti. 46 Ndipo Nebukadreza, mfalme, akaanguka kifudifudi, akamsujudia Danielii, akatoa amri wamtolee Danielii sadaka na uvumba. 47 Mfalme akajibu, akamwambia Danielii, Hakika Mungu wenu ndiye Mungu wa miungu, na Bwana wa wafalme, awezaye kufumbua siri, kwa kuwa wewe uliweza kuifumbua siri hii. 48 Basi mfalme akamtukuza Danielii, akampa zawadi kubwa nyingi sana, akamfanya kuwa mkubwa juu ya uliwali wote wa Babeli, na kuwa liwali mkuu juu ya wote wenye hekima wa Babeli. 49 Tena, Danielii akamwomba mfalme, naye akawaweka Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wawe juu ya mambo yote ya uliwali wa Babeli; lakini huyo Danielii alikuwa akiketi katika lango la mfalme.

Danieli 3

1 Nebukadreza, mfalme, alifanya sanamu ya dhahabu, ambayo urefu wake ulikuwa ni dhiraa sitini, na upana wake dhiraa sita; akaisimamisha katika uwanda wa Dura, katika wilaya ya Babeli. 2 Ndipo Nebukadreza akatuma watu kuwakusanya maamiri, na manaibu, na maliwali, na makadhi, na watunza hazina, na mawaziri, na mawakili, na wakuu wa wilaya zote, ili wahudhurie wakati wa kuizindua ile sanamu, mfalme Nebukadneza aliyoisimamisha. 3 Ndipo maamiri, na manaibu, na maliwali, na makadhi, na watunza hazina, na mawaziri, na mawakili, na wakuu wa wilaya zote, wakakusanyika ili kuizindua ile sanamu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha; wakasimama mbele ya ile sanamu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha. 4 Ndipo mpiga mbiu akapiga kelele akisema, Enyi watu wa kabila zote, na taifa, na lugha, mmeamriwa hivi, 5 wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, lazima kuanguka na kuiabudu sanamu ya dhahabu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha. 6 Na kila mtu asiyeanguka na kuabudu atatupwa saa iyo hiyo katika tanuru ya moto uwakao. 7 Basi wakati huo, watu wa kabila zote walipoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, watu wote na mataifa na lugha wakaanguka, wakaiabudu ile sanamu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha. 8 Basi baadhi ya Wakaldayo wakakaribia, wakaleta mashitaka juu ya Wayahudi. 9 Wakajibu, wakamwambia mfalme Nebukadreza, Ee mfalme, uishi milele. 10 Wewe, Ee mfalme, ulitoa amri ya kwamba kila mtu atakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, ni lazima aanguke na kuiabudu ile sanamu ya dhahabu; 11 na kila mtu asiyeanguka na kuabudu atatupwa katika tanuru ya moto uwakao. 12 Wako Wayahudi kadha wa kadha uliowaweka juu ya mambo ya wilaya ya Babeli, yaani, Shadraka, na Meshaki, na Abednego; watu hawa, Ee mfalme, hawakukujali wewe; hawaitumikii miungu yako, wala kuiabudu ile sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha. 13 Basi Nebukadreza akatoa amri kwa hasira na ghadhabu, waletwe hao Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Basi wakawaleta watu hao mbele ya mfalme. 14 Nebukadreza akajibu, akawaambia, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, je! Ni kwa makusudi hata hammtumikii mungu wangu wala kuisujudia sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha? 15 Basi sasa, kama mkiwa tayari wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, kuanguka na kuisujudia sanamu niliyoisimamisha, ni vema; bali msipoisujudia, mtatupwa saa iyo hiyo katika tanuru iwakayo moto; naye ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu? 16 Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakajibu, wakamwambia mfalme, Ee Nebukadreza, hamna haja kukujibu katika neno hili. 17 Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. 18 Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha. 19 Ndipo Nebukadreza akajaa ghadhabu, na sura ya uso wake ikabadilika juu ya Shadraka, na Meshaki, na Abednego, basi akatoa amri watie moto ile tanuru mara saba kuliko desturi yake ya kutiwa moto. 20 Kisha akawaamuru baadhi ya watu mashujaa wa jeshi lake kuwafunga Shadraka, na Meshaki, na Abednego, na kuwatupa katika ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. 21 Basi watu hao wakafungwa, hali wamevaa suruali zao, na kanzu zao, na joho zao, na mavazi yao mengine, wakatupwa katikati ya ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. 22 Basi kwa sababu amri ya mfalme ilikuwa ni kali, na ile tanuru ilikuwa ina moto sana, mwako wa ule moto ukawaua wale watu waliowashika Shadraka, na Meshaki, na Abednego. 23 Na watu hao watatu, Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakaanguka, hali wamefungwa, katikati ya ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. 24 Ndipo Nebukadreza akastaajabu, akainuka kwa haraka; akanena, akawaambia mawaziri wake, Je! Hatukutupa watu watatu, hali wamefungwa, katikati ya moto? Wakajibu, wakamwambia mfalme, Kweli, Ee mfalme. 25 Akajibu, akasema, Tazama, mimi naona watu wanne, nao wamefunguliwa, wanatembea katikati ya moto hali hawana dhara; na sura yake yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu. 26 Kisha Nebukadreza akaukaribia mdomo wa ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Akanena, akasema, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watumishi wa Mungu Aliye juu, tokeni, mje huku. Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakatoka katika ule moto. 27 Na maamiri, na manaibu, na maliwali, na mawaziri, waliokuwa wamekusanyika pamoja, wakawaona watu hao, ya kuwa ule moto ulikuwa hauna nguvu juu ya miili yao, wala nywele za vichwa vyao hazikuteketea, wala suruali zao hazikubadilika, wala harufu ya moto haikuwapata hata kidogo. 28 Nebukadreza akanena, akasema, Na ahimidiwe Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego; aliyemtuma malaika wake, akawaokoa watumishi wake waliomtumaini, wakaligeuza neno la mfalme, na kujitoa miili yao ili wasimtumikie mungu mwingine, wala kumwabudu, ila Mungu wao wenyewe. 29 Basi mimi naweka amri ya kuwa kila kabila ya watu, na kila taifa, na kila lugha, watakaonena neno lo lote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watakatwa vipande vipande, na nyumba zao zitafanywa jaa; kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii. 30 Kisha mfalme akawakuza Shadraka, na Meshaki, na Abednego, katika wilaya ya Babeli.

Danieli 4

1 Mfalme Nebukadreza, kwa watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wanaokaa katika dunia yote; Amani iongezeke kwenu. 2 Mimi nimeona vema kutangaza habari za ishara na maajabu, aliyonitendea Mungu aliye juu. 3 Ishara zake ni kubwa kama nini! Na maajabu yake yana uweza kama nini! Ufalme wake ni ufalme wa milele; na mamlaka yake ni ya kizazi hata kizazi. 4 Mimi, Nebukadreza, nalikuwa nikistarehe katika nyumba yangu, nikisitawi katika nyumba yangu ya enzi. 5 Nikaota ndoto iliyonitia hofu; mawazo niliyokuwa nayo kitandani mwangu, na njozi za kichwa changu, zikanifadhaisha. 6 Basi nikatoa amri kwamba wenye hekima wote wa Babeli, waletwe mbele yangu, ili kunijulisha tafsiri ya ndoto ile. 7 Ndipo wakaingia waganga, na wachawi, na Wakaldayo, na wanajimu; nikawahadithia ile ndoto; wao wasiweze kunijulisha tafsiri yake. 8 Bali hatimaye Danielii akaingia mbele yangu, ambaye jina lake ni Belteshaza, kwa kufuata jina la mungu wangu; tena ndani yake inakaa roho ya miungu watakatifu; nikamhadithia ile ndoto, nikisema, 9 Ee Belteshaza, mkuu wa waganga, kwa sababu ninajua ya kuwa roho ya miungu watakatifu inakaa ndani yako, na ya kuwa hapana neno la siri likushindalo, niambie njozi za ndoto yangu niliyoiona, na tafsiri yake. 10 Njozi za kichwa changu kitandani mwangu zilikuwa hivi; naliona, na tazama, palikuwa na mti katikati ya nchi, urefu wake mkubwa sana. 11 Mti ule ukakua, ukawa na nguvu, urefu wake ulifika mpaka mbinguni, na kuonekana kwake mpaka mwisho wa dunia. 12 Majani yake yalikuwa mazuri, na matunda yake mengi, na ndani yake chakula cha kuwatosha watu wote; wanyama wa kondeni walipata uvuli chini yake, na ndege wa angani walikaa katika matawi yake; kila kitu chenye mwili kilipata chakula kwake. 13 Nikaona katika njozi za kichwa changu kitandani mwangu, na tazama, mlinzi, naye ni mtakatifu, alishuka kutoka mbinguni. 14 Akapaza sauti yake, akasema, Ukateni mti huu, yafyekeni matawi yake, yapukusieni mbali majani yake, na kuyatawanya matunda yake, wanyama na waondoke hapo chini yake, na ndege katika matawi yake. 15 Walakini kiacheni kisiki cha shina lake katika ardhi, pamoja na pingu ya chuma na shaba, katika majani mororo ya kondeni; kikapate maji kwa umande wa mbinguni, na sehemu yake iwe pamoja na wanyama katika majani ya nchi; 16 moyo wake ubadilike, usiwe moyo wa binadamu, na apewe moyo wa mnyama; nyakati saba zikapite juu yake. 17 Hukumu hii imekuja kwa agizo la walinzi, na amri hii kwa neno la watakatifu; kusudi walio hai wapate kujua ya kuwa Aliye juu anatawala katika ufalme wa wanadamu, naye humpa amtakaye, tena humtawaza juu yake aliye mnyonge. 18 Mimi, Nebukadreza, nimeiona ndoto hii; na wewe, Ee Belteshaza, eleza tafsiri yake, kwa maana wenye hekima wote wa ufalme wangu hawawezi kunijulisha tafsiri yake; bali wewe waweza, maana roho ya miungu watakatifu inakaa ndani yako. 19 Ndipo Danielii, aliyeitwa jina lake Belteshaza, akashangaa kwa muda, na fikira zake zikamfadhaisha. Mfalme akajibu akasema, Ee Belteshaza, ndoto ile isikufadhaishe wala tafsiri yake. Belteshaza akajibu, akasema, Bwana wangu, ndoto hii iwapate wao wakuchukiao, na tafsiri yake iwapate adui zako. 20 Ule mti uliouona, uliokua, ukawa na nguvu, urefu wake ukafika mpaka mbinguni, na kuonekana kwake mpaka dunia yote; 21 ambao majani yake yalikuwa mazuri, na matunda yake mengi, na ndani yake chakula cha kuwatosha wote; ambao chini yake wanyama wa kondeni walikaa, na ndege wa angani walikuwa na makao yao katika matawi yake; 22 ni wewe, Ee mfalme, uliyekua, na kupata nguvu; maana ukuu wako umekua na kufika mpaka mbinguni, na mamlaka yako yamefika mpaka mwisho wa dunia. 23 Tena, kwa kuwa mfalme alimwona mlinzi, naye ni mtakatifu, akishuka kutoka mbinguni, akisema, Ukateni mti huu, mkauangamize; ila kiacheni kisiki cha shina lake katika ardhi, pamoja na pingu ya chuma na shaba, katika majani mororo ya kondeni; kikatiwe maji kwa umande wa mbinguni, na sehemu yake iwe pamoja na wanyama wa kondeni, hata nyakati saba zipite juu yake; 24 tafsiri yake ni hii, Ee mfalme, nayo ni amri yake Aliye juu, iliyomjia bwana wangu, mfalme; 25 ya kuwa utafukuzwa mbali na wanadamu, na makao yako yatakuwa pamoja na wanyama wa kondeni, nawe utalazimishwa kula majani kama ng'ombe, nawe utatiwa maji kwa umande wa mbinguni, na nyakati saba zitapita juu yako; hata utakapojua ya kuwa Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu, naye humpa yeye amtakaye, awaye yote. 26 Na kwa kuwa waliamuru kukiacha kisiki cha shina lake; ufalme wako utakuwa imara kwako, baada ya wewe kujua ya kuwa mbingu ndizo zinazotawala. 27 Kwa sababu hiyo, Ee mfalme, shauri langu lipate kibali kwako; ukaache dhambi zako kwa kutenda haki, ukaache maovu yako kwa kuwahurumia maskini; huenda ukapata kuzidishiwa siku zako za kukaa raha. 28 Hayo yote yakampata mfalme Nebukadreza. 29 Baada ya miezi kumi na miwili, alikuwa akitembea ndani ya jumba la kifalme katika Babeli. 30 Mfalme akanena, akasema, Mji huu sio Babeli mkubwa nilioujenga mimi, uwe kao langu la kifalme, kwa uwezo wa nguvu zangu, ili uwe utukufu wa enzi yangu? 31 Hata neno lile lilipokuwa katika kinywa cha mfalme, sauti ilikuja kutoka mbinguni, ikisema, Ee mfalme Nebukadreza, maneno haya unaambiwa wewe; Ufalme huu umeondoka kwako. 32 Nawe utafukuzwa mbali na wanadamu, na makao yako yatakuwa pamoja na wanyama wa kondeni; utalishwa majani kama ng'ombe, na nyakati saba zitapita juu yako, hata utakapojua ya kuwa Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu, naye humpa amtakaye, awaye yote. 33 Saa iyo hiyo jambo hilo likatimizwa, likampata Nebukadreza; alifukuzwa mbali na wanadamu, akala majani kama ng'ombe, na mwili wake ulilowa maji kwa umande wa mbinguni, hata nywele zake zikakua, zikawa kama manyoya ya tai, na kucha zake kama kucha za ndege. 34 Hata mwisho wa siku hizo, mimi, Nebukadreza, nikainua macho yangu kuelekea mbingu, fahamu zangu zikanirudia; nikamhimidi Yeye aliye juu, nikamsifu na kumheshimu Yeye aishiye milele; kwa maana mamlaka yake ni mamlaka ya milele, na ufalme wake hudumu toka kizazi hata kizazi; 35 na watu wote wanaokaa duniani wamehesabiwa kuwa si kitu, naye hufanya kama atakavyo, katika jeshi la mbinguni, na katika hao wanaokaa duniani; wala hapana awezaye kuuzuia mkono wake, wala kumwuliza, Unafanya nini wewe? 36 Basi wakati uo huo fahamu zangu zikanirudia, na kwa ajili ya utukufu wa ufalme wangu, enzi yangu na fahari yangu zikanirudia; na mawaziri wangu, na madiwani wangu, wakaja kunitafuta; nami nikathibitika katika ufalme wangu, nikaongezewa enzi kupita kiasi. 37 Basi mimi, Nebukadreza, namhimidi Mfalme wa mbinguni, namtukuza na kumheshimu; maana matendo yake yote ni kweli, na njia zake ni za adili; na wale waendao kwa kutakabari, yeye aweza kuwadhili.

Danieli 5

1 Belshaza, mfalme, aliwafanyia wakuu wake elfu karamu kubwa akanywa divai mbele ya elfu hao. 2 Belshaza, alipokuwa akionja ile divai, akaamuru wavilete vile vyombo vya dhahabu na fedha, ambavyo baba yake, Nebukadreza, alivitoa katika hekalu lililokuwako Yerusalemu; ili kwamba mfalme, na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wapate kuvinywea. 3 Basi wakavileta vile vyombo vya dhahabu, vilivyotolewa katika hekalu la nyumba ya Mungu lililokuwako Yerusalemu; na mfalme na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wakavinywea. 4 Wakanywa divai, wakaisifu miungu ya dhahabu, na ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe. 5 Saa iyo hiyo vikatokea vidole vya mkono wa mwanadamu, vikaandika katika chokaa ya ukuta wa nyumba ya enzi ya mfalme, mahali palipokikabili kinara; naye mfalme akakiona kitanga cha ule mkono ulioandika. 6 Ndipo uso wa mfalme ukambadilika; fikira zake zikamfadhaisha; viungo vya viuno vyake vikalegea; magoti yake yakagongana. 7 Mfalme akalia kwa sauti kubwa, akaamuru waletwe wachawi, na Wakaldayo na wanajimu. Mfalme akanena, akawaambia wenye hekima wa Babeli, mtu awaye yote atakayesoma maandiko haya, na kunionyesha tafsiri yake, atavikwa mavazi ya rangi ya zambarau, na kuwa na mkufu wa dhahabu shingoni mwake, naye atakuwa mtu wa tatu katika ufalme. 8 Basi wakaingia wenye hekima wote wa mfalme; lakini hawakuweza kuyasoma yale maandiko, wala kumjulisha mfalme tafsiri yake. 9 Ndipo mfalme Belshaza akahangaika sana, uso wake ukambadilika, na wakuu wake wakaona fadhaa. 10 Basi malkia, kwa sababu ya maneno ya mfalme na ya wakuu wake, akaingia katika nyumba ya karamu; malkia akanena, akasema, Ee mfalme, uishi milele; fikira zako zisikufadhaishe; wala uso wako usibadilike. 11 Yuko mtu katika ufalme wako, ambaye roho ya miungu watakatifu inakaa ndani yake; na katika siku za baba yako nuru na ufahamu na hekima zilionekana ndani yake; na mfalme Nebukadreza, baba yako, naam, mfalme, baba yako, akamfanya kuwa mkuu wa waganga, na wachawi, na Wakaldayo, na wanajimu; 12 kwa kuwa roho njema kupita kiasi, na maarifa, na ufahamu, na uwezo wa kufasiri ndoto, na kufunua maneno ya fumbo, na kufungua mafundo, zilionekana katika Danielii huyo, ambaye mfalme alimwita Belteshaza. Basi na aitwe Danielii, naye ataionyesha tafsiri. 13 Ndipo Danielii akaletwa mbele ya mfalme. Na Mfalme akanena, akamwambia Danielii, Je! Wewe ndiwe Danielii yule, aliye mmoja wa wana wa Yuda waliohamishwa, ambao mfalme, baba yangu, aliwaleta huku toka Yerusalemu? 14 Nimesikia habari zako, kwamba roho ya miungu imo ndani yako, na kwamba nuru na ufahamu na akili bora zimeonekana kwako. 15 Basi sasa, watu wenye hekima na wachawi wameletwa mbele yangu, wapate kulisoma andiko hili, na kunijulisha tafsiri yake; lakini hawakuweza kunijulisha tafsiri ya jambo hili. 16 Lakini nimesikia habari zako, kwamba waweza kuleta tafsiri, na kufumbua mafumbo; haya! Kama ukiweza kulisoma andiko hili, na kunijulisha tafsiri yake, utavikwa mavazi ya rangi ya zambarau, na kuwa na mkufu wa dhahabu shingoni mwako, nawe utakuwa mtu wa tatu katika ufalme. 17 Ndipo Danielii akajibu, akasema mbele ya mfalme; Zawadi zako zishike wewe mwenyewe; na thawabu zako mpe mtu mwingine; walakini nitamsomea mfalme maandiko haya, na kumjulisha tafsiri yake. 18 Kwa habari zako, Ee mfalme, Mungu Aliye juu alimpa Nebukadreza, baba yako, ufalme, na ukuu, na fahari, na utukufu; 19 na kwa sababu ya ule ukuu aliompa, watu wa kabila zote, na mataifa, na lugha, wakatetemeka na kuogopa mbele yake; aliyetaka kumwua alimwua; na aliyetaka kumwacha hai, alimwacha hai; aliyetaka kumtukuza, alimtukuza; na aliyetaka kumshusha, alimshusha. 20 Lakini moyo wake ulipoinuliwa, na roho yake ilipokuwa ngumu akatenda kwa kiburi, aliuzuliwa katika kiti chake cha enzi, nao wakamwondolea utukufu wake. 21 Akafukuzwa mbali na wanadamu, moyo wake ukafanywa kuwa kama moyo wa mnyama, na makao yake yalikuwa pamoja na punda-mwitu; akalishwa majani kama ng'ombe, mwili wake ukalowa maji kwa umande wa mbinguni; hata alipojua ya kuwa Mungu Aliye juu ndiye anayetawala katika ufalme wa wanadamu, na ya kuwa humweka juu yake yeye amtakaye, awaye yote. 22 Na wewe, mwanawe, Ee Belshaza, hukujinyenyekeza moyo wako, ijapokuwa ulijua hayo yote. 23 Bali umejiinua juu ya Bwana wa mbingu; nao wamevileta vyombo vya nyumba yake mbele yako; na wewe, na wakuu wako, na wake zako, na masuria wako, mmevinywea; nawe umeisifu miungu ya fedha na ya dhahabu na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe; wasioona, wala kusikia, wala kujua neno lo lote; na Mungu yule, ambaye pumzi yako i mkononi mwake, na njia zako zote ni zake, hukumtukuza. 24 Ndipo kile kitanga cha ule mkono kikaletwa kutoka mbele zake, na maandiko haya yameandikwa. 25 Na maandiko yaliyoandikwa ni haya; MENE, MENE, TEKELI, NA PERESI. 26 Na tafsiri ya maneno haya ni hii; MENE, Mungu ameuhesabu ufalme wako na kuukomesha. 27 TEKELI, umepimwa katika mizani nawe umeonekana kuwa umepunguka. 28 PERESI, ufalme wako umegawanyika, nao wamepewa Wamedi na Waajemi. 29 Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvika Danielii mavazi ya rangi ya zambarau, wakatia mkufu wa dhahabu shingoni mwake, wakapiga mbiu kutangaza habari zake, ya kwamba yeye ni mtu wa tatu katika ufalme. 30 Usiku uo huo Belshaza, mfalme wa Wakaldayo, akauawa. 31 Na Dario, Mmedi, akaupokea ufalme, naye umri wake alikuwa na miaka sitini na miwili.

Danieli 6

1 Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; 2 na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danielii alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. 3 Basi Danielii huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. 4 Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danielii kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake. 5 Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danielii huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake. 6 Basi wale mawaziri na maamiri wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia hivi, Mfalme Dario, uishi milele. 7 Mawaziri wote wa ufalme, na manaibu, na maamiri, na madiwani, na maliwali wamefanya shauri pamoja ili kuweka amri ya kifalme; na kupiga marufuku, ya kwamba mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme atatupwa katika tundu la simba. 8 Sasa, Ee mfalme, piga marufuku, ukatie sahihi maandiko haya, yasibadilike, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kubadilika. 9 Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku. 10 Hata Danielii, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. 11 Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danielii akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake. 12 Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika. 13 Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danielii, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku. 14 Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danielii; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa. 15 Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. 16 Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danielii, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danielii, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. 17 Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danielii. 18 Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. 19 Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. 20 Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danielii kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danielii, Ee Danielii, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? 21 Ndipo Danielii akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. 22 Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. 23 Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danielii katika lile tundu. Ndipo Danielii akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. 24 Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danielii, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. 25 Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. 26 Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danielii; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho. 27 Yeye huponya na kuokoa, hutenda ishara na maajabu mbinguni na duniani, ndiye aliyemponya Danielii na nguvu za simba. 28 Basi Danielii huyo akafanikiwa katika enzi ya Dario, na katika enzi ya Koreshi, Mwajemi.

Danieli 7

1 Katika mwaka wa kwanza wa Belshaza, mfalme wa Babeli, Danielii aliona ndoto, na maono ya kichwa chake, kitandani mwake; basi akaiandika ndoto, akatoa habari ya jumla ya mambo hayo. 2 Danielii akanena, akisema, Naliona katika maono yangu wakati wa usiku; na tazama, hizo pepo nne za mbinguni zilivuma kwa nguvu juu ya bahari kubwa. 3 Ndipo wanyama wakubwa wanne wakatoka baharini, wote wa namna mbalimbali. 4 Wa kwanza alikuwa kama simba, naye alikuwa na mabawa ya tai; nikatazama, hata mabawa yake yakafutuka manyoya, akainuliwa katika nchi, akasimamishwa juu kwa miguu miwili kama mwanadamu; naye akapewa moyo wa kibinadamu. 5 Na tazama, mnyama mwingine, wa pili, kama dubu, naye aliinuliwa upande mmoja, na mifupa mitatu ya mbavu ilikuwamo kinywani mwake katika meno yake; wakamwambia mnyama huyo hivi, Inuka, ule nyama tele. 6 Kisha nikatazama, na kumbe! Mnyama mwingine, kama chui, naye juu ya mgongo wake alikuwa na mabawa manne kama ya ndege; mnyama huyo alikuwa na vichwa vinne; akapewa mamlaka. 7 Baadaye nikaona katika njozi ya usiku, na tazama, mnyama wa nne, mwenye kutisha, mwenye nguvu, mwenye uwezo mwingi, naye alikuwa na meno ya chuma, makubwa sana; alikula na kuvunja vipande vipande, na kuyakanyaga mabaki kwa miguu yake; na umbo lake lilikuwa mbali kabisa na wale wa kwanza, naye alikuwa na pembe kumi. 8 Nikaziangalia sana pembe zake, na tazama, pembe nyingine ikazuka kati yao, nayo ilikuwa ndogo, ambayo mbele yake pembe tatu katika zile za kwanza zikang'olewa kabisa; na tazama, katika pembe hiyo mlikuwa na macho kama macho ya mwanadamu, na kinywa kilichokuwa kikinena maneno makuu. 9 Nikatazama hata viti vya enzi vikawekwa, na mmoja aliye mzee wa siku ameketi; mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji, na nywele za kichwa chake kama sufu safi; kiti chake cha enzi kilikuwa miali ya moto, na gurudumu zake moto uwakao. 10 Mto kama wa moto ukatoka ukapita mbele zake; maelfu elfu wakamtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi wakasimama mbele zake; hukumu ikawekwa, na vitabu vikafunuliwa. 11 Nikatazama wakati huo; kwa sababu ya sauti ya yale maneno makubwa iliyoyasema ile pembe; nalitazama hata mnyama yule akauawa, mwili wake ukaharibiwa, akatolewa ateketezwe kwa moto. 12 Na kwa habari za wale wanyama wengine, walinyang'anywa mamlaka yao; walakini maisha yao yalidumishwa kwa wakati na majira. 13 Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. 14 Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa. 15 Basi, mimi Danielii, roho yangu ilihuzunika mwilini mwangu, na hayo maono ya kichwa changu yakanifadhaisha. 16 Nikamkaribia mmoja wa hao waliosimama karibu, nikamwuliza maana ya kweli ya hayo yote. Basi akaniambia, akanijulisha tafsiri ya mambo hayo. 17 Wanyama hao wakubwa walio wanne ni wafalme wanne watakaotokea duniani. 18 Lakini watakatifu wake Aliye juu wataupokea ufalme, na kuumiliki huo ufalme milele, naam hata milele na milele. 19 Kisha nalitaka kujua maana ya yule mnyama wa nne, aliyekuwa mbali na wenziwe wote, mwenye kutisha sana, ambaye meno yake yalikuwa ya chuma, na makucha yake ya shaba; aliyekula, na kuvunja vipande vipande, na kuyakanyaga mabaki kwa miguu yake; 20 na habari za zile pembe kumi zilizokuwa kichwani mwake, na ile pembe nyingine iliyozuka, ambayo mbele yake zilianguka pembe tatu; yaani, pembe ile yenye macho, na kanwa lililonena makuu, ambayo kuonekana kwake kulikuwa hodari kuliko wenzake. 21 Nikatazama, na pembe iyo hiyo ilifanya vita na watakatifu, ikawashinda; 22 hata akaja huyo mzee wa siku, nao watakatifu wake Aliye juu wakapewa hukumu; na majira yakawadia watakatifu waumiliki ufalme. 23 Akanena hivi, Huyo mnyama wa nne atakuwa ni ufalme wa nne juu ya dunia, utakaokuwa mbali na falme zile zote, nao utakula dunia yote, na kuikanyaga, na kuivunja vipande vipande. 24 Na habari za zile pembe kumi, katika ufalme huo wataondoka wafalme kumi; na mwingine ataondoka baada ya hao; naye atakuwa mbali na hao wa kwanza; naye atawashusha wafalme watatu. 25 Naye atanena maneno kinyume chake Aliye juu, naye atawadhoofisha watakatifu wake Aliye juu; naye ataazimu kubadili majira na sheria; nao watatiwa mikononi mwake kwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati. 26 Lakini hukumu itawekwa, nao watamwondolea mamlaka yake, kuipoteza na kuiangamiza, hata milele. 27 Na ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu; ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamtumikia na kumtii. 28 Huu ndio mwisho wa jambo lile. Nami, Danielii, fikira zangu zilinifadhaisha, na uso wangu ulinibadilika; lakini naliliweka jambo hilo moyoni mwangu.

Danieli 8

1 Katika mwaka wa tatu wa kumiliki kwake mfalme Belshaza maono yalinitokea mimi, naam, mimi Danielii, baada ya hayo yaliyonitokea hapo kwanza. 2 Nami naliona katika maono; ilitukia, nilipoona, nalikuwako huko Shushani ngomeni, katika wilaya ya Elamu; nikaona katika maono, nami nalikuwa karibu na mto Ulai. 3 Ndipo nikainua macho yangu nikaona, na tazama, mbele ya mto alisimama kondoo mume, mwenye pembe mbili; na pembe zile mbili zilikuwa ndefu; lakini moja ilikuwa ndefu kuliko ya pili, na ile iliyokuwa ndefu zaidi ilizuka mwisho. 4 Nikamwona huyo kondoo mume akisukuma upande wa magharibi, na upande wa kaskazini, na upande wa kusini; wala hakuna mnyama ye yote awezaye kusimama mbele yake, wala hakuna mnyama ye yote awezaye kupokonya mkononi mwake; lakini alitenda kama alivyopenda mwenyewe, akajitukuza nafsi yake. 5 Nami nilipokuwa nikifikiri, tazama, beberu akatoka upande wa magharibi, juu ya uso wa dunia nzima, bila kuigusa nchi; na beberu yule alikuwa na pembe mashuhuri kati ya macho yake. 6 Naye akamwendea huyo kondoo mume mwenye pembe mbili, niliyemwona akisimama karibu na mto, akamshambulia kwa ghadhabu za nguvu zake. 7 Nikamwona akimkaribia kondoo mume, akamwonea hasira kali, akampiga kondoo mume, akazivunja pembe zake mbili; na huyo kondoo mume alikuwa hana nguvu kusimama mbele yake; bali akamwangusha chini, akamkanyaga-kanyaga; wala hapakuwapo awezaye kumwokoa kondoo mume katika mkono wake. 8 Na yule beberu akajitukuza sana; na alipokuwa na nguvu, pembe ile kubwa ilivunjika; na badala yake zikazuka pembe nne mashuhuri zilizoelekea pepo nne za mbinguni. 9 Na katika moja ya pembe hizo ilitokea pembe ndogo, iliyokua sana, upande wa kusini, na upande wa magharibi, na upande wa nchi ya uzuri. 10 Nayo ikakua, kiasi cha kulifikilia jeshi la mbinguni; ikaangusha chini baadhi ya jeshi lile, na ya nyota, ikazikanyaga. 11 Naam, ikajitukuza hata juu yake aliye mkuu wa jeshi hilo, ikamwondolea sadaka ya kuteketezwa ya daima, na mahali pa patakatifu pake pakaangushwa chini. 12 Na jeshi likatolewa kwake pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya daima, kwa sababu ya makosa; nayo ikaiangusha kweli hata chini; ikatenda ilivyopenda, na kufanikiwa. 13 Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kuteketezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi? 14 Akamwambia, Hata nyakati za jioni na asubuhi elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakapotakaswa. 15 Ikawa mimi, naam, mimi Danielii, nilipoyaona maono hayo, nalitafuta kuyafahamu, na tazama, alisimama mbele yangu mmoja mfano wa mwanadamu. 16 Nikasikia sauti ya mwanadamu katikati ya mto Ulai, iliyoita na kusema, Gabrieli, mfahamishe mtu huyu maono haya. 17 Basi alipakaribia mahali niliposimama; nami naliogopa alipokaribia, nikaanguka kifudifudi; lakini aliniambia, Fahamu, Ee mwanadamu, kwa maana maono haya ni ya wakati wa mwisho. 18 Basi alipokuwa akisema nami, nalishikwa na usingizi mzito na uso wangu uliielekea nchi; lakini alinigusa, akanisimamisha wima. 19 Akaniambia, Tazama, nitakujulisha yatakayokuwa wakati wa mwisho wa ghadhabu; maana, ni ya wakati wa mwisho ulioamriwa. 20 Yule kondoo mume uliyemwona, mwenye pembe mbili, hizo ndizo wafalme wa Umedi na Uajemi. 21 Na yule beberu, mwenye manyoya mengi, ni mfalme wa Uyunani; na ile pembe kubwa iliyo kati ya macho yake ni mfalme wa kwanza. 22 Tena katika habari ya pembe ile iliyovunjika, ambayo badala yake zilisimama pembe nne, falme nne zitasimama kutoka katika taifa lile, lakini si kwa nguvu kama zake. 23 Na wakati wa mwisho wa ufalme wao, wakosao watakapotimia, mfalme mwenye uso mkali, afahamuye mafumbo, atasimama. 24 Na nguvu zake zitakuwa nyingi mno, lakini si kwa uwezo wake mwenyewe; naye ataharibu kiasi cha kustaajabisha watu, na kufanikiwa, na kutenda apendavyo; naye atawaangamiza hao walio hodari na watu watakatifu. 25 Na kwa mashauri yake atafanikisha hila mkononi mwake; naye atajitukuza nafsi yake moyoni mwake; naye atawaangamiza wengi katika hali yao ya salama; naye atasimama kushindana naye aliye Mkuu wa wakuu; lakini atavunjika, bila kazi ya mikono. 26 Na maono ya hizo nyakati za jioni na asubuhi yaliyosemwa ni kweli; lakini wewe yafunike maono hayo; maana ni ya wakati ujao baada ya siku nyingi. 27 Na mimi, Danielii, nikazimia, nikaugua siku kadha wa kadha; kisha nikaondoka, nikatenda shughuli za mfalme; nami naliyastajabia yale maono, ila hakuna aliyeyafahamu.

Danieli 9

1 Katika mwaka wa kwanza wa Dario, mwana wa Ahasuero, wa uzao wa Wamedi, aliyetawazwa kuwa mfalme juu ya milki ya Wakaldayo; 2 katika mwaka wa kwanza wa kumiliki kwake, mimi Danielii, kwa kuvisoma vitabu, nalifahamu hesabu ya miaka, ambayo neno la Bwana lilimjia Yeremia nabii, ya kuutimiza ukiwa wa Yerusalemu, yaani, miaka sabini. 3 Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na majivu. 4 Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake; 5 tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; 6 wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, na watu wote wa nchi. 7 Ee Bwana, haki ina wewe, lakini kwetu sisi kuna haya ya uso, kama hivi leo; kwa watu wa Yuda, na kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa Israeli wote, walio karibu na hao walio mbali, katika nchi zote ulikowafukuza, kwa sababu ya makosa yao waliyokukosa. 8 Ee Bwana, kwetu sisi kuna haya ya uso, kwa wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, kwa sababu tumekutenda dhambi. 9 Rehema na msamaha ni kwa Bwana Mungu wetu, ingawa tumemwasi; 10 wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii. 11 Naam, Israeli wote wameihalifu sheria yako, kwa kugeuka upande, wasiisikilize sauti yako; basi kwa hiyo laana imemwagwa juu yetu, na uapo ule ulioandikwa katika sheria ya Musa, mtumishi wa Mungu; kwa sababu tumemtenda dhambi. 12 Naye ameyathibitisha maneno yake, aliyoyanena juu yetu, na juu ya waamuzi wetu waliotuamua, kwa kumletea mambo maovu makuu; maana chini ya mbingu zote halikutendeka jambo kama hili, lilivyotendeka juu ya Yerusalemu. 13 Kama ilivyoandikwa katika sheria ya Musa, mabaya haya yote yametupata lakini hata hivyo hatukumwomba Bwana, Mungu wetu, atupe fadhili zake, ili tugeuke na kuyaacha maovu yetu, na kuitambua kweli yake. 14 Basi Bwana ameyavizia mabaya hayo, akatuletea; maana Bwana, Mungu wetu ni mwenye haki katika kazi zake zote azitendazo; na sisi hatukuitii sauti yake. 15 Na sasa, Ee Bwana Mungu wetu, uliyewatoa watu wako hawa katika nchi ya Misri kwa mkono hodari, ukajipatia sifa, kama ilivyo leo; tumefanya dhambi, tumetenda maovu. 16 Ee Bwana sawasawa na haki yako yote, nakusihi, hasira yako na ghadhabu yako zigeuzwe na kuuacha mji wako Yerusalemu, mlima wako mtakatifu; maana kwa sababu ya dhambi zetu, na maovu ya baba zetu, Yerusalemu na watu wako wamepata kulaumiwa na watu wote wanaotuzunguka. 17 Basi sasa, Ee Mungu wetu, yasikilize maombi ya mtumishi wako, na dua zake, ukaangazishe uso wako juu ya patakatifu pako palipo ukiwa, kwa ajili ya Bwana. 18 Ee Mungu wangu, tega sikio lako, ukasikie; fumbua macho yako ukautazame ukiwa wetu, na mji ule ulioitwa kwa jina lako; maana hatukutolei maombi yetu kwa sababu ya haki yetu, lakini kwa sababu ya rehema zako nyingi. 19 Ee Bwana, usikie; Ee Bwana, usamehe; Ee Bwana, usikilize, ukatende, usikawie; kwa ajili yako wewe, Ee Mungu wangu; kwa sababu mji wako na watu wako wanaitwa kwa jina lako. 20 Basi hapo nilipokuwa nikisema, na kuomba, na kuiungama dhambi yangu, na dhambi ya watu wangu Israeli, na kuomba dua yangu mbele za Bwana, Mungu wangu, kwa ajili ya mlima mtakatifu wa Mungu wangu; 21 naam, nilipokuwa nikinena katika kuomba, mtu yule, Gabrieli, niliyemwona katika njozi hapo kwanza, akirushwa upesi, alinigusa panapo wakati wa dhabihu ya jioni. 22 Akaniagiza, akaongea nami, akasema, Ee Danielii, nimetokea sasa, ili nikupe akili upate kufahamu. 23 Mwanzo wa maombi yako ilitolewa amri, nami nimekuja kukupasha habari; maana wewe unapendwa sana; basi itafakari habari hii, na kuyafahamu maono haya. 24 Muda wa majuma sabini umeamriwa juu ya watu wako, na juu ya mji wako mtakatifu, ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu, na kuleta haki ya milele, na kutia muhuri maono na unabii, na kumtia mafuta yeye aliye mtakatifu. 25 Basi ujue na kufahamu, ya kuwa tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata zamani zake masihi aliye mkuu; kutakuwa na majuma saba; na katika majuma sitini na mawili utajengwa tena pamoja na njia kuu zake na handaki, naam, katika nyakati za taabu. 26 Na baada ya yale majuma sitini na mawili, masihi atakatiliwa mbali, naye atakuwa hana kitu; na watu wa mkuu atakayekuja watauangamiza mji, na patakatifu; na mwisho wake utakuwa pamoja na gharika, na hata mwisho ule vita vitakuwapo; ukiwa umekwisha kukusudiwa. 27 Naye atafanya agano thabiti na watu wengi kwa muda wa juma moja; na kwa nusu ya juma hiyo ataikomesha sadaka na dhabihu; na mahali pake litasimama chukizo la uharibifu; na hivyo, hata ukomo, na ghadhabu iliyokusudiwa imemwagwa juu yake mwenye kuharibu.

Danieli 10

1 Katika mwaka wa tatu wa Koreshi, mfalme wa Uajemi, Danielii, ambaye jina lake aliitwa Belteshaza, alifunuliwa neno; na neno lile lilikuwa kweli; maana ni vita vikubwa; naye akalifahamu neno lile, akaelewa na maono hayo. 2 Katika siku zile mimi, Danielii, nalikuwa nikiomboleza muda wa majuma matatu kamili. 3 Sikula chakula kitamu, wala nyama wala divai haikuingia kinywani mwangu, wala sikujipaka mafuta kabisa, hata majuma matatu kamili yalipotimia. 4 Na siku ya ishirini na nne ya mwezi wa kwanza, nilipokuwa kando ya ule mto mkubwa, Hidekeli; 5 naliinua macho yangu, nikatazama, na kumbe, mtu aliyevikwa nguo za kitani, viuno vyake vimefungwa dhahabu safi ya Ufazi; 6 mwili wake pia ulikuwa kama zabarajadi safi, na uso wake mfano wa umeme, na macho yake kama taa za moto, na mikono yake na miguu yake rangi yake kama shaba iliyosuguliwa sana, na sauti ya maneno yake kama sauti ya umati wa watu. 7 Nami, Danielii, nikaona maono haya peke yangu; maana wale watu waliokuwa pamoja nami hawakuyaona maono haya; lakini tetemeko kuu liliwashika, hata wakakimbia ili kujificha. 8 Basi nikaachwa peke yangu, nikaona maono haya makubwa, wala hazikubaki nguvu ndani yangu; maana uzuri wangu uligeuzwa ndani yangu kuwa uharibifu, wala sikusaziwa nguvu. 9 Walakini naliisikia sauti ya maneno yake; nami niliposikia sauti ya maneno yake, ndipo nikashikwa na usingizi mzito, na uso wangu umeielekea nchi. 10 Na tazama, mkono ukanigusa, ukaniweka juu ya magoti yangu, na vitanga vya mikono yangu. 11 Akaniambia, Ee Danielii, mtu upendwaye sana, yafahamu maneno nikuambiayo, ukasimame kiwima-wima; maana kwako nimetumwa sasa. Na aliponiambia neno hili, nalisimama nikitetemeka. 12 Ndipo akaniambia, Usiogope, Danielii; kwa maana tangu siku ile ya kwanza ulipotia moyo wako ufahamu, na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, maneno yako yalisikiwa; nami nimekuja kwa ajili ya maneno yako. 13 Lakini mkuu wa ufalme wa Uajemi alinipinga siku ishirini na moja; bali, tazama, huyo Mikaeli, mmoja wa hao wakuu wa mbele, akaja kunisaidia; nami nikamwacha huko pamoja na wafalme wa Uajemi. 14 Sasa nimekuja kukufahamisha mambo yatakayowapata watu wako katika siku za mwisho; maana maono hayo ni ya siku nyingi bado. 15 Na alipokwisha kusema nami maneno hayo, nikauelekeza uso wangu chini, nikawa bubu. 16 Na kumbe, mmoja mfano wa wanadamu akanigusa midomo yangu; ndipo nikafumbua kinywa changu, nikanena, nikamwambia yeye aliyesimama karibu nami, Ee Bwana wangu, kwa sababu ya maono haya huzuni zangu zimenipata tena; hata sikusaziwa nguvu. 17 Maana, mtumishi wa Bwana wangu huyu atawezaje kusema na Bwana wangu huyu? Kwa maana kwangu mimi, mara hazikusalia nguvu ndani yangu, wala pumzi haikusalia ndani yangu. 18 Kisha mmoja mfano wa mwanadamu akanigusa tena, akanitia nguvu. 19 Akasema, Ee mtu upendwaye sana, usiogope; amani na iwe kwako, uwe na nguvu, naam, uwe na nguvu. Aliposema nami nikapata nguvu, nikasema, Ee Bwana wangu, na aseme Bwana wangu; kwa maana umenitia nguvu. 20 Ndipo akasema, Je! Unajua sababu hata nikakujia? Na sasa nitarudi ili nipigane na mkuu wa Uajemi; nami nitakapotoka huku, tazama, mkuu wa Uyunani atakuja. 21 Lakini nitakuambia yaliyoandikwa katika maandiko ya kweli; wala hapana anisaidiaye juu ya hao ila huyo Mikaeli, mkuu wenu.

Danieli 11

1 Tena mimi, katika mwaka wa kwanza wa Dario, Mmedi, mimi nalisimama nimthibitishe na kumtia nguvu. 2 Nami sasa nitakuonyesha yaliyo kweli. Tazama, watasimama wafalme watatu katika Uajemi; naye mfalme wa nne atakuwa tajiri kuliko hao wote; naye atakapopata nguvu kwa utajiri wake, atawachochea wote juu ya ufalme wa Uyunani. 3 Na mfalme hodari atasimama, atakayetawala kwa mamlaka kubwa, na kutenda apendavyo. 4 Naye atakaposimama, ufalme wake utavunjika, na kugawanyika katika pepo nne za mbinguni; lakini hautakuwa wa uzao wake, wala hautakuwa kama mamlaka yake ambayo alitawala kwayo; kwa maana ufalme wake utang'olewa, hata kwa ajili ya wengine zaidi ya hao. 5 Na mfalme wa kusini atakuwa hodari; na mmoja wa wakuu wake atakuwa hodari kuliko yeye, naye atakuwa na mamlaka; mamlaka yake itakuwa mamlaka kubwa. 6 Na baada ya miaka kadha wa kadha watashirikiana; kwa kuwa binti wa mfalme wa kusini atakuja kwa mfalme wa kaskazini, ili kufanya mapatano naye; lakini hatakuwa na nguvu za mkono wake sikuzote; wala mfalme yule hatasimama, wala mkono wake; lakini yule binti atatolewa, na hao waliomleta, na yeye aliyemzaa, na yeye aliyemtia nguvu, zamani zile. 7 Lakini katika chipukizi la mizizi yake atasimama mmoja mahali pake atakayeliendesha jeshi la askari, naye ataingia katika ngome ya mfalme wa kaskazini, na kuwatenda mambo, na kuwashinda; 8 na miungu yao, pamoja na sanamu zao, na vyombo vyao vizuri vya fedha na dhahabu atavichukua mpaka Misri; kisha atajizuia miaka kadha wa kadha asimwendee mfalme wa kaskazini. 9 Naye huyo ataingia katika ufalme wa mfalme wa kusini, lakini atarudi mpaka nchi yake mwenyewe. 10 Na wanawe watafanya vita, na kukusanya mkutano wa majeshi makuu; watakaokuja na kufurika na kupita katikati; nao watarudi na kufanya vita mpaka penye ngome yake. 11 Na mfalme wa kusini ataingiliwa na ghadhabu, naye atatoka na kupigana naye, yaani, na mfalme wa kaskazini; naye atapanga jeshi kubwa; na jeshi hilo litawekwa mikononi mwake. 12 Atakapokwisha kuchukua lile jeshi, moyo wake utatukuzwa; naye atawaangusha makumi elfu; lakini hataongezewa nguvu. 13 Kwa maana mfalme wa kaskazini atarudi, naye atapanga jeshi kubwa kuliko lile la kwanza; naye hakika atakuja mwisho wa zamani zile, yaani, baada ya miaka kadha wa kadha, pamoja na jeshi kubwa na mali nyingi. 14 Na zamani zile watu wengi watasimama ili kumpinga mfalme wa kusini; pia, wenye jeuri miongoni mwa watu wako watajiinua ili kuyathibitisha maono; lakini wataanguka. 15 Basi mfalme wa kaskazini atakuja, na kufanya kilima, na kuupiga mji wenye maboma; na silaha za kusini hazitaweza kumpinga, wala watu wake wateule, wala hapatakuwa na nguvu za kumpinga. 16 Maana ajaye kupigana naye atatenda kadiri apendavyo, wala hapana mtu atakayesimama mbele yake; naye atasimama katika nchi ya uzuri, na uharibifu utakuwa mkononi mwake. 17 Naye atakaza uso wake ili aje pamoja na nguvu zote za ufalme wake, naye atafanya mapatano naye; naye atatenda kadiri apendavyo; naye atampa binti wa watu ili amharibu; lakini hilo halitasimama wala kumfaa. 18 Baada ya hayo atauelekeza uso wake kwenye visiwa, naye atavipiga visiwa vingi; lakini mkuu mmoja ataikomesha aibu iliyoletwa na yeye; naam, aibu yake hiyo atamrudishia mwenyewe. 19 Ndipo atauelekeza uso wake kwenye ngome za nchi yake mwenyewe; lakini atajikwaa na kuanguka, wala hataonekana tena. 20 Ndipo badala yake atasimama mmoja, atakayepitisha mwenye kutoza ushuru kati ya utukufu wa ufalme wake; lakini katika muda wa siku chache ataangamizwa, si kwa hasira, wala si katika vita. 21 Kisha badala yake atasimama mmoja, mtu astahiliye kudharauliwa, ambaye hawakumpa heshima ya ufalme; naye atakuja wakati wa amani, naye ataupata ufalme kwa kujipendekeza. 22 Na wale wenye silaha mfano wa gharika watagharikishwa mbele yake, na kuvunjika, naam, mkuu wa maagano pia. 23 Na baada ya maagano atatenda kwa hila; maana atapanda, naye atakuwa hodari pamoja na watu wadogo. 24 Wakati wa amani atapaingia mahali palipofanikiwa sana pa wilaya hiyo; naye atatenda mambo ambayo baba zake hawakuyatenda, wala babu zake; atatawanya kati yao mawindo, na mateka, na mali; naam, atatunga hila zake juu ya ngome, hata wakati ulioamriwa. 25 Naye atachochea nguvu zake na ushujaa wake juu ya huyo mfalme wa kusini kwa jeshi kubwa; na mfalme wa kusini atafanya vita kwa jeshi kubwa mno lenye nguvu nyingi; lakini hatasimama; maana watatunga hila juu yake. 26 Naam, walao sehemu ya chakula chake watamwangamiza, na jeshi lake litagharikishwa; na wengi wataanguka wameuawa. 27 Na katika habari za wafalme hao wawili, mioyo yao watanuia kutenda madhara, nao watasema uongo walipo pamoja mezani; lakini hilo halitafanikiwa; maana mwisho utatokea wakati ulioamriwa. 28 Ndipo atakaporudi mpaka nchi yake mwenye utajiri mwingi; na moyo wake utakuwa kinyume cha hilo agano takatifu; naye atafanya kama apendavyo, na kurudi mpaka nchi yake. 29 Kwa wakati ulioamriwa atarudi, na kuingia upande wa kusini; lakini wakati wa mwisho mambo hayatakuwa kama yalivyokuwa wakati wa kwanza. 30 Maana merikebu za Kitimu zitakuja kupigana naye; basi atavunjika moyo, naye atarudi na kulighadhibikia hilo agano takatifu; na kutenda kadiri apendavyo; naam, atarudi, na kuwasikiliza walioacha hilo agano takatifu. 31 Na wenye silaha watasimama upande wake, nao watapatia unajisi mahali patakatifu, ndiyo ngome, nao wataondoa sadaka ya kuteketezwa ya kila siku, nao watalisimamisha chukizo la uharibifu. 32 Na wao wafanyao maovu juu ya hilo agano atawapotosha kwa maneno ya kujipendekeza; lakini watu wamjuao Mungu wao watakuwa hodari, na kutenda mambo makuu. 33 Na hao walio wenye hekima katika watu watafundisha wengi; hata hivyo wataanguka kwa upanga, na kwa moto, na kwa kufungwa, na kwa kutekwa nyara, siku nyingi. 34 Basi watakapoanguka, watasaidiwa kwa msaada kidogo; lakini wengi wataambatana nao kwa maneno ya kujipendekeza. 35 Na baadhi yao wenye hekima wataanguka, ili kuwatakasa, na kuwasafisha, na kuwafanya weupe, hata wakati wa mwisho; kwa maana ni kwa wakati ulioamriwa, ambao haujaja. 36 Naye mfalme atafanya kama apendavyo; naye atajitukuza na kujiadhimisha juu ya kila mungu, naye atanena maneno ya ajabu juu ya Mungu wa miungu, naye atafanikiwa mpaka ghadhabu itakapotimia; maana yaliyokusudiwa yatafanyika. 37 Wala hataijali miungu ya baba zake; wala yeye aliyetamaniwa na wanawake; wala hatamjali mungu awaye yote; maana atajitukuza mwenyewe juu ya wote. 38 Lakini katika mahali pake atamheshimu mungu wa ngome; na mungu ambaye baba zake hawakumjua atamheshimu, kwa dhahabu, na fedha, na vito vya thamani, na vitu vipendezavyo. 39 Naye ataziteka nyara ngome zenye nguvu kwa msaada wa mungu mgeni; na yeye atakayemkubali atamwongeza kwa utukufu; naye atawapa kumiliki wengi; naye ataigawa nchi kwa rushwa, 40 na wakati wa mwisho mfalme wa kusini atashindana naye; na mfalme wa kaskazini atamshambulia kama upepo wa kisulisuli, pamoja na magari ya vita, na wapanda farasi, na merikebu nyingi; naye ataingia katika nchi hizo, na kufurika na kupita katikati. 41 Tena ataingia katika hiyo nchi ya uzuri, na nchi nyingi zitapinduliwa; lakini nchi hizi zitaokolewa na mkono wake, Edomu, na Moabu, na wakuu wa watu wa Amoni. 42 Naye ataunyosha mkono wake juu ya nchi hizo, hata na nchi ya Misri haitaokoka. 43 Lakini atakuwa na nguvu juu ya hazina za dhahabu na fedha, na juu ya vitu vyote vya Misri vyenye thamani; na Walibia na Wakushi watafuata nyayo zake. 44 Lakini habari zitokazo mashariki na kaskazini zitamfadhaisha; naye atatoka kwa ghadhabu nyingi, ili kuharibu, na kuwaondolea mbali watu wengi. 45 Naye ataweka hema zake za kifalme kati ya bahari na mlima mtakatifu wa uzuri; lakini ataifikilia ajali yake, wala hakuna atakayemsaidia.

Danieli 12

1 Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile. 2 Tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele. 3 Na walio na hekima watang'aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang'aa kama nyota milele na milele. 4 Lakini wewe, Ee Danielii, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa yataongezeka. 5 Ndipo mimi, Danielii, nikatazama, na kumbe, wamesimama wengine wawili, mmoja ukingoni mwa mto upande huu, na mmoja ukingoni mwa mto upande wa pili. 6 Na mmoja akamwuliza yule mtu aliyevikwa nguo za kitani, aliyekuwa juu ya maji ya mto, Je! Itakuwa muda wa miaka mingapi hata mwisho wa mambo haya ya ajabu? 7 Nami nikamsikia yule mtu aliyevikwa nguo za kitani, aliyekuwa juu ya maji ya mto, hapo alipoinua mkono wake wa kuume na mkono wake wa kushoto kuelekea mbinguni; akaapa kwa yeye aliye hai milele na milele, ya kwamba itakuwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati; tena watakapokuwa wamekwisha kuvunja nguvu za hao watu watakatifu, ndipo mambo hayo yote yatakapotimizwa. 8 Nami nikasikia, lakini sikuelewa; ndipo nikasema, Ee Bwana wangu, mwisho wa mambo haya utakuwaje? 9 Akasema, Enenda zako, Danielii; maana maneno haya yamefungwa, na kutiwa muhuri, hata wakati wa mwisho. 10 Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika; bali wabaya watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; bali wao walio na hekima ndio watakaoelewa. 11 Na tangu wakati ule ambapo sadaka ya kuteketezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu litakaposimamishwa, itapata siku elfu na mia mbili na tisini. 12 Heri angojaye, na kuzifikilia siku hizo elfu na mia tatu na thelathini na tano. 13 Lakini enenda zako hata utakapokuwa mwisho ule; maana wewe utastarehe, nawe utasimama katika kura yako mwisho wa siku hizo.

Hosea 1

1 Hili ndilo neno la Bwana lililomjia Hosea, mwana wa Beeri, siku za Uzia, na Yothamu, na Ahazi, na Hezekia, wafalme wa Yuda; na siku za Yeroboamu, mwana wa Yoashi, mfalme wa Israeli. 2 Hapo kwanza Bwana aliponena kwa kinywa cha Hosea, Bwana alimwambia Hosea, Enenda ukatwae mke wa uzinzi, na watoto wa uzinzi; kwa maana nchi hii inafanya uzinzi mwingi, kwa kumwacha Bwana. 3 Basi akaenda akamwoa Gomeri, binti Diblaimu; naye akachukua mimba, akamzalia mtoto mwanamume. 4 Bwana akamwambia, Mwite jina lake Yezreeli; kwa maana bado kitambo kidogo, nitaipatiliza nyumba ya Yehu damu ya Yezreeli, na kuukomesha ufalme wa nyumba ya Israeli. 5 Tena itakuwa siku ile, nitauvunja upinde wa Israeli katika bonde la Yezreeli. 6 Akachukua mimba tena, akazaa mtoto mwanamke. Bwana akamwambia, Mwite jina lake Lo-ruhama kwa maana sitairehemu nyumba ya Israeli tena,nisije nikawasamehe kwa njia yoyote. 7 Lakini nitairehemu nyumba ya Yuda; nitawaokoa kwa Bwana, Mungu wao; wala sitawaokoa kwa upinde, wala kwa upanga, wala kwa silaha, wala kwa farasi, wala kwa wapanda farasi. 8 Basi, akiisha kumwachisha Lo-ruhama, akachukua mimba, akazaa mtoto mwanamume. 9 Bwana akasema, Mwite jina lake Lo-ami kwa maana ninyi si watu wangu,wala mimi sitakuwa MUNGU wenu. 10 Tena itakuwa ya kwamba hesabu ya wana wa Israeli itafanana na mchanga wa bahari, usioweza kupimwa wala kuhesabiwa; tena itakuwa, badala ya kuambiwa, Ninyi si watu wangu, wataambiwa, Ninyi ndio wana wa Mungu aliye hai. 11 Na wana wa Yuda na wana wa Israeli watakusanyika pamoja, nao watajiwekea kichwa kimoja, nao watakwea watoke katika nchi hii; kwa maana siku ya Yezreeli itakuwa kuu sana.

Hosea 2

1 Waambieni ndugu zenu wanaume, Ami na ndugu zenu wanawake, Ruhama. 2 Msihini mama yenu, msihini; kwa maana yeye si mke wangu, wala mimi si mume wake; na ayawekee mbali mambo ya uasherati wake yasiwe mbele ya uso wake, na mambo ya uzinzi wake yasiwe kati ya maziwa yake; 3 nisije nikamvua nguo zake akawa uchi, nikamweka katika hali aliyokuwa nayo siku ya kuzaliwa kwake, na kumfanya kama jangwa, na kumweka kama nchi kame, na kumfisha kwa kiu; 4 naam, sitawaonea rehema watoto wake; kwa maana ni watoto wa uzinzi. 5 Maana mama yao amezini; yeye aliyewachukua mimba ametenda mambo ya aibu; maana alisema, Nitafuatana na wapenzi wangu, wanipao chakula changu na maji yangu, sufu yangu na kitani yangu, mafuta yangu na vileo vyangu. 6 Basi kwa ajili ya hayo, angalia, nitaiziba njia yako kwa miiba, nami nitafanya kitalu juu yake, asipate kuyaona mapito yake. 7 Naye atawafuata wapenzi wake, lakini hatawapata; atawatafuta, lakini hatawaona; ndipo atakaposema, Nitakwenda nikamrudie mume wangu wa kwanza; kwa maana hali yangu ya zamani ilikuwa njema kuliko hali yangu ya sasa. 8 Maana hakujua ya kuwa mimi ndiye aliyempa ngano, na divai, na mafuta, na kumwongezea fedha na dhahabu, walivyovitumia kwa ajili ya Baali. 9 Basi kwa ajili ya hayo, nitaitwaa tena ngano yangu kwa wakati wake, na divai yangu kwa wakati wake, nami nitamnyang'anya sufu yangu na kitani yangu, vya kumfunika uchi wake. 10 Na sasa nitaifunua aibu yake mbele ya macho ya wapenzi wake, wala hapana mtu atakayemwokoa katika mkono wangu. 11 Tena nitaikomesha furaha yake yote, na sikukuu zake, na siku zake za mwandamo wa mwezi, na sabato zake, na makusanyiko yake yote yaliyoamriwa. 12 Nami nitaiharibu mizabibu yake na mitini yake, ambayo alisema, Hii ndiyo ujira wangu niliopewa na wapenzi wangu; nami nitaifanya kuwa msitu, na wanyama wa mashamba wataila. 13 Nami nitamwadhibu kwa sababu ya siku za Mabaali, aliowafukizia uvumba; hapo alipojipamba kwa pete masikioni mwake, na kwa vito asema Bwana. 14 Kwa hiyo angalia, mimi nitamshawishi, na kumleta nyikani, na kusema naye maneno ya kumtuliza moyo. 15 Nami nitampa mashamba yake ya mizabibu toka huko, na bonde la Akori kuwa mlango wa tumaini; naye ataniitikia huko, kama siku zile za ujana wake, na kama siku ile alipopanda kutoka nchi ya Misri. 16 Tena siku hiyo itakuwa, asema Bwana, utaniita Ishi 17 Kwa maana nitayaondoa majina ya Mabaali kinywani mwake, wala hawatatajwa tena kwa majina yao. 18 Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; nami nitavivunja upinde na upanga na silaha vitoke katika nchi, nami nitawalalisha salama salimini. 19 Nami nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na kwa ufadhili, na kwa rehema. 20 Nami nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua Bwana. 21 Tena itakuwa siku hiyo, mimi nitaitika, asema Bwana; nitaziitikia mbingu, nazo zitaiitikia nchi; 22 nayo nchi itaiitikia nafaka na divai na mafuta; nayo yataiitikia Yezreeli. 23 Nami nitampanda katika nchi kwa ajili yangu mwenyewe; nami nitamrehemu yeye asiyepewa rehema; nami nitawaambia wale wasiokuwa watu wangu, Ninyi ndinyi watu wangu; nao watasema, Wewe ndiwe Mungu wangu.

Hosea 3

1 Bwana akaniambia, Enenda tena, mpende mwanamke apendwaye na rafiki yake, naye ni mzinzi; kama vile Bwana awapendavyo wana wa Israeli, ingawa wanaigeukia miungu mingine, na kupenda mikate ya zabibu kavu. 2 Basi nikajinunulia mwanamke huyo kwa vipande kumi na vitano vya fedha, na homeri moja ya shayiri, na nusu ya homeri ya shayiri; 3 nami nilimwambia, Utatawa kwa ajili yangu siku nyingi; hutafanya mambo ya ukahaba, wala hutakuwa mke wa mtu awaye yote; nami nitakuwa hali iyo hiyo kwa ajili yako. 4 Kwa maana wana wa Israeli watakaa siku nyingi bila mfalme, wala mtu mkuu, wala sadaka, wala nguzo, wala naivera, wala kinyago; 5 baada ya hayo wana wa Israeli watarejea, na kumtafuta Bwana, Mungu wao, na Daudi, mfalme wao; nao watamwendea Bwana na wema wake kwa kicho siku za mwisho.

Hosea 4

1 Lisikieni neno la Bwana, enyi wana wa Israeli; kwa maana Bwana ana mateto nao wakaao katika nchi, kwa sababu hapana kweli, wala fadhili, wala kumjua Mungu katika nchi. 2 Hapana neno ila kuapa kwa uongo, na kuvunja ahadi, na kuua, na kuiba, na kuzini; huruka mpaka, na damu hugusana na damu. 3 Kwa ajili ya hayo nchi itaomboleza, na kila mtu akaaye ndani yake atadhoofika, pamoja na wanyama wa kondeni na ndege wa angani; naam, samaki wa baharini pia wataondolewa. 4 Walakini asishindane mtu, wala mtu asikemee; maana watu wako ni kama wao washindanao na kuhani. 5 Na wewe utajikwaa wakati wa mchana, na nabii naye atajikwaa pamoja nawe wakati wa usiku; nami nitamwangamiza mama yako. 6 Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako. 7 Kadiri walivyozidishwa, kwa kadiri iyo hiyo walinitenda dhambi; nami nitageuza utukufu wao kuwa aibu. 8 Hujilisha dhambi ya watu wangu, hujifurahisha moyo kwa uovu wao. 9 Hata itakuwa, kama walivyo watu, ndivyo atakavyokuwa kuhani; nami nitawaadhibu kwa ajili ya njia zao, na kuwalipa kwa matendo yao. 10 Nao watakula, lakini hawatashiba; watafanya zinaa, lakini hawataongezeka; kwa sababu wameacha kumwangalia Bwana. 11 Uzinzi na divai na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu. 12 Watu wangu hutaka shauri kwa gongo lao, na fimbo yao huwahubiri mambo; maana roho ya uzinzi imewakosesha, nao wamekwenda kuzini mbali na Mungu wao. 13 Hutoa dhabihu juu ya vilele vya milima, na kufukiza uvumba juu ya vilima, chini ya mialoni na milibua na miela, kwa kuwa uvuli wake ni mwema; kwa sababu hiyo binti zenu huzini, na bibi arusi zenu hufanya uasherati. 14 Sitawaadhibu binti zenu wazinipo, wala bibi arusi zenu wafanyapo uasherati; maana wao wenyewe huenda kando pamoja na wanawake wazinzi, hutoa dhabihu pamoja na makahaba; na watu hawa wasiofahamu wataangamia. 15 Ingawa wewe, Israeli, unafanya uzinzi, lakini asiasi Yuda; nanyi msiende Gilgali wala msipande mpaka Beth-Aveni, wala msiape mkisema, Aishivyo Bwana. 16 Kwa maana Israeli ametenda kwa ukaidi, kama ndama mkaidi; sasa je! Bwana atawalisha kama mwana-kondoo katika mahali penye nafasi! 17 Efraimu amejiungamanisha na sanamu; mwache. 18 Kileo chao kimegeuka kuwa uchungu; huzini daima; wakuu wake hupenda aibu. 19 Upepo umemfunikiza kwa mbawa zake; nao watatahayarika kwa sababu ya dhabihu zao.

Hosea 5

1 Sikieni haya, enyi makuhani, sikilizeni, enyi nyumba ya Israeli, tegeni masikio yenu, enyi wa nyumba ya mfalme, kwa kuwa hukumu hii yawahusu ninyi; maana mmekuwa mtego huko Mizpa, na wavu uliotandwa juu ya Tabori. 2 Nao walioasi wameongeza sana ufisadi wao; lakini mimi ndiye awakaripiaye wote pia. 3 Mimi namjua Efraimu, wala Israeli hakufichwa nisimwone; maana sasa, Ee Efraimu, umefanya uzinzi; Israeli ametiwa unajisi. 4 Matendo yao hayatawaacha kumgeukia Mungu wao; maana roho ya uzinzi imo ndani yao, wala hawamjui Bwana. 5 Na kiburi cha Israeli chamshuhudia mbele ya uso wake; kwa sababu hiyo, Israeli na Efraimu watajikwaa katika uovu wao. Yuda naye atajikwaa pamoja nao. 6 Watakwenda na makundi yao ya kondoo na ng'ombe wamtafute Bwana; lakini hawatamwona; amejitenga nao. 7 Wametenda kwa hila juu ya Bwana; maana wamezaa wana wageni; sasa mwezi huu uandamao utawala pamoja na mashamba yao. 8 Pigeni tarumbeta katika Gibea, na baragumu katika Rama; pazeni sauti ya hofu katika Beth-Aveni; nyuma yako, Ee Benyamini! 9 Efraimu atakuwa ukiwa siku ya kukemewa; katika kabila za Israeli nimetangaza habari itakayotokea halafu bila shaka. 10 Wakuu wa Yuda ni kama watu waondoao alama ya mpaka; nitawamwagia ghadhabu yangu kama maji. 11 Efraimu ameonewa, amesetwa katika hukumu, kwa sababu alikuwa radhi kufuata ubatili. 12 Kwa sababu hiyo mimi nimekuwa kama nondo kwa Efraimu, nimekuwa kama ubovu kwa nyumba ya Yuda. 13 Efraimu alipouona ugonjwa wake, na Yuda jeraha yake, ndipo Efraimu alipokwenda kwa Ashuru, akatuma watu kwa mfalme Yarebu; lakini yeye hawezi kuwapoza, wala hatawaponya jeraha yenu. 14 Maana mimi nitakuwa kama simba kwa Efraimu, na kama mwana-simba kwa nyumba ya Yuda; mimi, naam, mimi nitararua, kisha nitakwenda zangu; nitachukulia mbali, wala hapatakuwa na mtu wa kupokonya. 15 Nitakwenda zangu niparudie mahali pangu, hata watakapoungama makosa yao na kunitafuta uso wangu; katika taabu yao watanitafuta kwa bidii.

Hosea 6

1 Njoni, tumrudie Bwana; maana yeye amerarua, na yeye atatuponya; yeye amepiga, na yeye atatufunga jeraha zetu. 2 Baada ya siku mbili atatufufua; siku ya tatu atatuinua, nasi tutaishi mbele zake. 3 Nasi na tujue, naam, tukaendelee kumjua Bwana; kutokea kwake ni yakini kama asubuhi; naye atatujilia kama mvua, kama mvua ya vuli iinyweshayo nchi. 4 Ee Efraimu, nikutendee nini? Ee Yuda, nikutendee nini? Kwa maana fadhili zenu ni kama wingu la asubuhi na kama umande utowekao mapema. 5 Kwa sababu hiyo nimewakata-kata kwa vinywa vya manabii; nimewaua kwa maneno ya kinywa changu; na hukumu yangu itatokea kama mwanga. 6 Maana nataka fadhili wala si sadaka; na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa. 7 Lakini wao wamelivunja hilo agano kama Adamu; huko wamenitenda mambo ya hiana. 8 Gileadi ni mji wa hao watendao maovu, umetiwa rangi ya damu. 9 Na kama vile makundi ya wanyang'anyi wamwoteavyo mtu, ndivyo kundi la makuhani wauavyo katika njia ielekeayo Shekemu; naam, wametenda mambo maovu sana. 10 Katika nyumba ya Israeli nimeona jambo bovu kabisa; huko uzinzi umeonekana katika Efraimu; Israeli ametiwa unajisi. 11 Tena, Ee Yuda, wewe umeandikiwa mavuno, hapo nitakapowarudisha wafungwa wa watu wangu.

Hosea 7

1 Wakati nitakapo kumponya Israeli, ndipo yafunuliwapo maovu ya Efraimu, na ubaya wa Samaria; maana wanatenda uongo, na mwivi huvunja nyumba za watu, na kundi la wanyang'anyi hushambulia nje. 2 Wala hawafikiri mioyoni mwao ya kwamba naukumbuka uovu wao wote; sasa matendo yao wenyewe yamewazunguka pande zote; yako mbele za uso wangu. 3 Humfurahisha mfalme kwa uovu wao, na wakuu wao kwa uongo wao. 4 Hao wote ni wazinzi; wamekuwa kama tanuu iliyotiwa moto na mwokaji; huacha kuuchochea moto, tangu kuukanda unga hata umekwisha kutiwa chachu. 5 Sikukuu ya mfalme wetu, wakuu walijitapisha kwa ukali wa divai; alinyosha mkono wake pamoja na wenye mzaha. 6 Maana wamefanya moyo wao kuwa tayari kama tanuu, wakati waoteapo; hasira yao hulala usiku kucha; asubuhi yawaka kama moto utoao miali. 7 Wote wamepata moto kama tanuu, nao hula makadhi wao; wafalme wao wote wameanguka; hakuna hata mmoja wao aniitaye mimi. 8 Efraimu ajichanganya na mataifa; Efraimu ni mkate usiogeuzwa. 9 Wageni wamekula nguvu zake, naye hana habari; naam, nywele za mvi zimeonekana huko na huko juu yake, naye hana habari. 10 Na kiburi cha Israeli chamshuhudia mbele ya uso wake; ila hata hivyo hawakumrudia Bwana, Mungu wao, wala hawakumtafuta kwa ajili ya hayo yote. 11 Naye Efraimu amekuwa kama njiwa mpumbavu, asiye na fahamu; humwita Misri, huenda Ashuru. 12 Watakapokwenda nitatandika wavu wangu juu yao; nitawashusha kama ndege wa angani; nitawarudi, kama vile mkutano wao ulivyosikia. 13 Ole wao! Kwa kuwa wamenikimbia; uharibifu na uwapate! Kwa kuwa wameniasi; ingawa ninataka kuwakomboa, hata hivyo wamenena uongo juu yangu. 14 Wala hawakunililia kwa moyo, lakini wanalalamika vitandani mwao; hujikutanisha ili kupata nafaka na divai; huniasi mimi. 15 Ingawa nimewafundisha na kuwatia nguvu mikono yao, hata hivyo hukusudia udhalimu juu yangu. 16 Wao hurudi, lakini si kwake Aliye juu; wamekuwa kama upinde usiotumainika; wakuu wao wataanguka kwa upanga, kwa sababu ya jeuri ya ndimi zao; jambo hili litakuwa kwao sababu ya kuchekwa katika nchi ya Misri.

Hosea 8

1 Tia baragumu kinywani mwako. Kama tai, anakuja juu ya nyumba ya Bwana; kwa sababu wamelihalifu agano langu, wameiasi sheria yangu. 2 Watanililia, Mungu wangu, sisi Israeli tunakujua. 3 Israeli ameyatupa yaliyo mema; adui watamfuatia. 4 Wamesimamisha wafalme, lakini si kwa shauri langu; wamejifanyia wakuu, lakini nalikuwa sina habari; kwa fedha yao na dhahabu yao wamejifanyizia sanamu, kusudi wakatiliwe mbali. 5 Amemtupa ndama yako, Ee Samaria; hasira yangu imewaka juu yao; siku ngapi zitapita kabla ya hao kupata hali isiyo na hatia? 6 Maana katika Israeli kimetokea hata na kitu hiki; fundi ndiye aliyekifanya, nacho si mungu kamwe; naam, ndama ya Samaria itavunjika vipande vipande. 7 Kwa maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani; nafaka haina bua; machipuko yake hayatoi masuke; hata ikiwa yatoa, wageni watayameza. 8 Israeli amemezwa; sasa wamo miongoni mwa mataifa kama chombo kisichopendeza. 9 Kwa maana wamekwea kwenda Ashuru, mfano wa punda wa mwituni aliye peke yake; Efraimu ameajiri wapenzi. 10 Naam, ijapokuwa waajiri kati ya mataifa, sasa nitawakusanya; nao wanaanza kupunguka kwa sababu ya mzigo wa mfalme wa wakuu. 11 Kwa kuwa Efraimu ameongeza madhabahu kwa dhambi, madhabahu zimekuwa dhambi kwake. 12 Nijapomwandikia sheria yangu katika amri elfu kumi, zimehesabiwa kuwa ni kitu kigeni. 13 Kwa habari za dhabihu za matoleo yangu, hutoa dhabihu ya nyama na kuila; lakini Bwana hawakubali; sasa ataukumbuka uovu wao, na kuwapatiliza dhambi zao; watarudi kwenda Misri. 14 Maana Israeli amemsahau Muumba wake, naye amejenga nyumba za enzi; na Yuda ameongeza miji yenye maboma; lakini nitapeleka moto juu ya miji yake, nao utaziteketeza ngome zake.

Hosea 9

1 Usifurahi, Israeli, kwa sababu ya furaha, kama hao mataifa; kwa kuwa umezini juu ya Mungu wako, umependa ujira katika kila sakafu ya nafaka. 2 Sakafu na shinikizo hazitawalisha, na divai mpya itampungukia. 3 Hawatakaa katika nchi ya Bwana; lakini Efraimu atarudi Misri, nao watakula chakula kinajisi katika Ashuru. 4 Hawatammiminia Bwana divai, wala hazitampendeza sadaka zao; mkate wao utakuwa kama chakula cha matanga kwao; wote watakaokila watatiwa unajisi; kwa maana mkate wao utakuwa kwa shauku zao; hautaingia katika nyumba ya Bwana. 5 Mtafanya nini katika siku ya mkutano wa idi, na katika siku ya karamu ya Bwana? 6 Kwa maana, tazama, wamekwenda zao ili kukimbia uharibifu, lakini Misri itawakusanya, Nofu itawazika; vitu vyao vya fedha viwapendezavyo, magugu yatavimiliki; miiba itakuwa katika hema zao. 7 Siku za kupatilizwa zimekuja, siku za kulipa zimefika; Israeli atayajua hayo; huyo nabii ni mpumbavu, huyo mtu mwenye roho ana wazimu; kwa sababu ya wingi wa uovu wako, na kwa sababu uadui umekuwa mkubwa. 8 Efraimu alikuwa mlinzi pamoja na Mungu wangu; na huyo nabii, mtego wa mwinda ndege u katika njia zake zote; katika nyumba ya Mungu wake umo uadui. 9 Wamejiharibu mno, kama katika siku za Gibea; ataukumbuka uovu wao, atazilipiza dhambi zao. 10 Mimi nalimkuta Israeli kama zabibu nyikani; nami naliwaona baba zenu kama matunda ya mtini yaliyoiva kwanza, wakati wake wa kwanza; lakini walikwenda Baal-Peori, wakajiweka wakfu kwa kitu cha aibu, wakawa chukizo kama kitu kile walichokipenda. 11 Naye Efraimu, utukufu wake utarukia mbali kama ndege, uzazi hautakuwako, wala aliye na mimba, wala achukuaye mimba. 12 Wajapolea watoto wao, mimi nitawanyang'anya watoto wao, asisalie hata mtu mmoja; naam, ole wao! Nitakapoondoka na kuwaacha. 13 Efraimu amepandwa mahali pazuri, kama nilivyoona Tiro; lakini Efraimu atamtolea mwuaji watoto wake. 14 Wape, Ee Bwana; utawapa kitu gani? Wape tumbo lenye kuharibu mimba na maziwa makavu. 15 Uovu wao wote u katika Gilgali; maana huko naliwachukia; kwa sababu ya uovu wa matendo yao nitawafukuza watoke katika nyumba yangu; sitawapenda tena; wakuu wao wote ni waasi. 16 Efraimu amepigwa; mzizi wao umekauka; hawatazaa matunda; naam, wajapozaa, nitaliua tunda la tumbo lipendwalo sana. 17 Mungu wangu atawatupilia mbali, kwa sababu hawakumsikiliza; nao watakuwa watu wa kutanga-tanga kati ya mataifa.

Hosea 10

1 Israeli ni mzabibu, utoao matunda yake; kwa kadiri ya wingi wa matunda yake, kwa kadiri iyo hiyo ameongeza madhabahu zake; kwa kadiri ya wema wa nchi yake, kwa kadiri iyo hiyo wamefanya nguzo nzuri. 2 Moyo wao umegawanyika; sasa wataonekana kuwa na hatia; yeye atazipiga madhabahu zao, ataziharibu nguzo zao. 3 Yakini sasa watasema, Hatuna mfalme; kwa maana hatumchi Bwana; na mfalme huyu je! Aweza kututendea nini? 4 Hunena maneno yasiyo na maana; huapa kwa uongo wafanyapo maagano; basi ndipo hukumu huchipuka kama mbaruti katika matuta ya shamba. 5 Wakaao Samaria wataona hofu kwa ajili ya ndama za Beth-Aveni; kwa maana watu wa mji huo wataulilia, na makuhani wake walioufurahia, kwa sababu ya utukufu wake; kwa maana umetoweka. 6 Nayo itachukuliwa Ashuru, iwe zawadi kwa mfalme Yarebu; Efraimu atapata aibu, na Israeli atalionea haya shauri lake mwenyewe. 7 Katika habari za Samaria, mfalme wake amekatiliwa mbali, kama povu usoni pa maji. 8 Mahali pa Aveni palipoinuka, yaani, dhambi ya Israeli, pataharibika; mwiba na mbigili itamea juu ya madhabahu zake; nao wataiambia milima, Tusitirini; na vilima, Tuangukieni. 9 Ee Israeli, umefanya dhambi tangu siku za Gibea; huko ndiko walikosimama; ili vita vilivyokuwa juu ya wana wa uovu visiwapate katika Gibea. 10 Wakati nitakapopenda nitawaadhibu; na hao mataifa watakusanyika juu yao, watakapofungwa kwa sababu ya makosa yao mawili. 11 Naye Efraimu ni ndama aliyefundishwa, apendaye kupura; lakini nimepitisha kongwa juu ya shingo yake nzuri; nitampandisha mwenye kupanda juu ya Efraimu; Yuda atalima, na Yakobo atavunja madongoa yake. 12 Jipandieni katika haki, vuneni kwa fadhili; uchimbueni udongo wa mashamba yenu, kwa maana wakati umewadia wa kumtafuta Bwana, hata atakapokuja na kuwanyeshea haki. 13 Mmelima dhuluma, mmevuna uovu; mmekula matunda ya uongo; kwa maana uliitumainia njia yako, na wingi wa mashujaa wako. 14 Kwa sababu hiyo fitina itatokea kati ya watu wako, na ngome zako zote zitaharibiwa, kama vile Shalmani alivyoharibu Betharbeli, katika siku ya vita; mama akavunjika-vunjika pamoja na watoto wake. 15 Hivyo ndivyo Betheli atakavyowatenda ninyi, kwa sababu ya ubaya wenu mwingi; wakati wa mapambazuko mfalme wa Israeli atakatiliwa mbali kabisa.

Hosea 11

1 Israeli alipokuwa mtoto, nalikuwa nikimpenda, nikamwita mwanangu atoke Misri. 2 Kadiri walivyowaita ndivyo walivyoondoka na kuwaacha; waliwatolea dhabihu Mabaali, na kuzifukizia uvumba sanamu za kuchonga. 3 Lakini nalimfundisha Efraimu kwenda kwa miguu; naliwachukua mikononi mwangu; hawakujua ya kuwa naliwaponya. 4 Naliwavuta kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo; nami nalikuwa kwao kama hao waondoao kongwa tayani mwao, nikaandika chakula mbele yao. 5 Hatarudi tena nchi ya Misri; bali huyo Mwashuri atakuwa mfalme wake; kwa sababu walikataa kurejea. 6 Na upanga utaiangukia miji yake, utayaharibu makomeo yake na kuyala, kwa sababu ya mashauri yao wenyewe. 7 Na watu wangu wamejipinda kuniacha; ingawa wawaita kwenda kwake Aliye juu, hapana hata mmoja atakayemtukuza. 8 Niwezeje kukuacha, Efraimu? Niwezeje kukuponya, Israeli? Niwezeje kukufanya kama Adma? Niwezeje kukuweka kama Seboimu ? Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zimewaka pamoja. 9 Sitatumia ukali wa hasira yangu, sitarudi kumwangamiza Efraimu; kwa maana mimi ni Mungu, si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia ndani ya mji. 10 Watakwenda kumfuata Bwana, atakayenguruma kama simba; kwa maana atanguruma, nao watoto watakuja kutoka magharibi wakitetemeka. 11 Watakuja wakitetemeka kama shomoro, toka Misri, na kama hua, toka nchi ya Ashuru; nami nitawakalisha katika nyumba zao, asema Bwana. 12 Efraimu amenizinga kwa maneno ya uongo, na nyumba ya Israeli kwa udanganyifu; na Yuda hata sasa anasita-sita kwa Mungu, na kwake aliye Mtakatifu, naye ni mwaminifu.

Hosea 12

1 Efraimu hujilisha upepo, na kuandamana na upepo wa mashariki; haachi kuongeza uongo na uharibifu; nao wafanya agano na Ashuru, na mafuta huchukuliwa kwenda Misri. 2 Bwana naye ana mateto na Yuda, naye atamwadhibu Yakobo kwa kadiri ya njia zake; kwa kadiri ya matendo yake atamlipa. 3 Tumboni alimshika ndugu yake kisigino; Na alipokuwa mtu mzima alikuwa na uwezo kwa Mungu; 4 Naam, alikuwa na uwezo juu ya malaika Akashinda; alilia, na kumsihi; Alimwona huko Betheli, naye akasema nasi huko; 5 Naam, Bwana, Mungu wa majeshi; Bwana ndilo kumbukumbu lake. 6 Basi, mrudie Mungu wako; shika fadhili na hukumu; ukamngojee Mungu wako daima. 7 Ni mchuuzi, mizani ya udanganyifu i mkononi mwake; anapenda kudhulumu. 8 Naye Efraimu alisema, Kweli nimekuwa tajiri, nimejipatia mali nyingi; katika kazi zangu zote hawataona kwangu uovu wo wote uliokuwa dhambi. 9 Lakini mimi ni Bwana, Mungu wako tangu ulipotoka katika nchi ya Misri; nitakukalisha tena katika hema, kama siku za karamu ya idi. 10 Tena nimenena na hao manabii, nami nimeongeza maono, na kwa utumishi wa manabii nimetumia mifano. 11 Je! Gileadi ni uovu? Wamekuwa ubatili tu; huko Gilgali hutoa dhabihu za ng'ombe; naam, madhabahu zao zimekuwa kama chungu katika matuta ya mashamba. 12 Na Yakobo alikimbia mpaka Padan-Aramu, Na Israeli alitumika apate mke; Ili apate mke alichunga kondoo. 13 Na kwa nabii Bwana alimtoa Israeli katika Misri, Na kwa mkono wa nabii alihifadhiwa. 14 Efraimu amenitia hasira kali sana; kwa sababu hiyo damu yake itaachwa juu yake, na Bwana wake atamrudishia lawama yake.

Hosea 13

1 Efraimu aliponena, palikuwa na tetemeko; alijitukuza katika Israeli; Lakini alipokosa katika Baali, alikufa. 2 Na sasa wanazidi kufanya dhambi, nao wamejifanyizia sanamu kwa fedha yao, naam, sanamu kwa kadiri ya akili zao; zote pia ni kazi ya mafundi; nao huzitaja hivi, Wanaume watoao dhabihu na wazibusu ndama. 3 Kwa sababu hiyo watakuwa kama wingu la asubuhi, na kama umande utowekao upesi, kama makapi yaliyopeperushwa na tufani sakafuni, na kama moshi utokao katika bomba. 4 Lakini mimi ni Bwana, Mungu wako tangu nchi ya Misri; wala hutamjua mungu mwingine ila mimi; wala zaidi ya mimi hakuna Mwokozi. 5 Mimi nalikujua katika jangwa, katika nchi yenye kiu nyingi. 6 Kwa kadiri ya malisho yao, kwa kadiri iyo hiyo walishiba; walishiba na moyo wao ukatukuka; ndiyo sababu wamenisahau mimi. 7 Basi nimekuwa kama simba kwao; kama chui nitavizia njiani; 8 nitakutana nao kama dubu aliyenyang'anywa watoto wake; nami nitararua nyama ya mioyo yao; na huko nitawala kama simba; huyo mnyama mkali atawararua. 9 Haya ndiyo maangamizo yako, Ee Israeli, ya kuwa wewe u kinyume changu mimi, kinyume cha msaada wako. 10 Yuko wapi sasa mfalme wako, apate kukuokoa katika miji yako yote? Na hao waamuzi wako, uliowanena hivi, Nipe mfalme na wakuu? 11 Nimekupa mfalme katika hasira yangu, nikamwondoa katika ghadhabu yangu. 12 Uovu wa Efraimu umefungwa kwa kukazwa; dhambi yake imewekwa akiba. 13 Utungu wa mwanamke mwenye mimba utampata; yeye ni mwana asiye na akili; maana wakati umewadia, ambao haimpasi kukawia mahali wapenyapo watoto. 14 Nitawakomboa na nguvu za kaburi; nitawaokoa na mauti; ewe mauti, ya wapi mapigo yako? Ewe kaburi, ku wapi kuharibu kwako? Kujuta kutafichwa na macho yangu. 15 Ajapokuwa yeye ni mwenye kuzaa sana kati ya ndugu zake, upepo wa mashariki utakuja, hiyo pumzi ya Bwana itokayo upande wa nyikani, na kijito chake cha maji kitakauka, na chemchemi yake itakaushwa; yeye atateka nyara hazina ya vyombo vyote vipendezavyo. 16 Samaria atachukua hatia yake; kwa maana amemwasi Mungu wake; wataanguka kwa upanga; watoto wao wachanga watavunjwa vipande vipande, na wanawake wao wenye mimba watatambuliwa.

Hosea 14

1 Ee Israeli, mrudie Bwana, Mungu wako; maana umeanguka kwa sababu ya uovu wako. 2 Chukueni maneno pamoja nanyi, mkamrudie Bwana; mkamwambie, Ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema; na hivyo ndivyo mtakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng'ombe. 3 Ashuru hatatuokoa; hatutapanda farasi; wala hatutaiambia tena kazi ya mikono yetu, Ninyi ndinyi miungu yetu; maana kwako wewe wasio na baba hupata rehema. 4 Mimi nitawaponya kurudi nyuma kwao; nitawapenda kwa ukunjufu wa moyo; kwa maana hasira yangu imemwacha. 5 Nitakuwa kama umande kwa Israeli; naye atachanua maua kama nyinyoro, na kuieneza mizizi yake kama Lebanoni. 6 Matawi yake yatatandaa, na uzuri wake utakuwa kama uzuri wa mzeituni, na harufu yake kama Lebanoni. 7 Na wao wakaao chini ya uvuli wake watarejea; watafufuka kama ngano, na kuchanua maua kama mzabibu; harufu yake itakuwa kama harufu ya divai ya Lebanoni. 8 Efraimu atasema, Mimi nina nini tena na sanamu? Mimi nimeitika, nami nitamwangalia. Mimi ni kama mberoshi wenye majani mabichi. Kwangu mimi yamepatikana matunda yako. 9 Ni nani aliye na hekima, naye atayafahamu mambo haya? Ni nani aliye na busara, naye atayajua? Kwa maana njia za Bwana zimenyoka, nao wenye haki watakwenda katika njia hizo; bali waasio wataanguka ndani yake.

Yoeli 1

1 Neno la Bwana lililomjia Yoeli, mwana wa Pethueli. 2 Sikieni haya, enyi wazee; Sikilizeni, enyi wenyeji wote wa nchi. Je! Mambo haya yamekuwako katika siku zenu, Au katika siku za baba zenu? 3 Waarifuni watoto wenu habari yake, Watoto wenu wakawaambie watoto wao, Na watoto wao wakakiambie kizazi kingine. 4 Yaliyosazwa na tunutu yameliwa na nzige; na yaliyosazwa na nzige yameliwa na parare; na yaliyosazwa na parare yameliwa na madumadu. 5 Levukeni, enyi walevi, mkalie; Pigeni yowe, ninyi nyote mnywao divai; Kwa sababu ya divai mpya; Maana umekatiliwa mbali na vinywa vyenu. 6 Maana taifa limepanda juu ya nchi yangu, Lenye nguvu, tena halina hesabu; Meno yake ni kama meno ya simba, Naye ana magego ya simba mkubwa. 7 Ameuharibu mzabibu wangu; ameuvunja mtini wangu; ameyaambua magamba yake kabisa; ameuangusha chini; matawi yake yamefanywa kuwa meupe. 8 Ombolea kama mwanamwali avaaye magunia Kwa ajili ya mume wa ujana wake. 9 Sadaka ya unga na sadaka ya kinywaji Zimekatiliwa mbali na nyumba ya Bwana; Hao makuhani, wahudumu wa Bwana, wanaomboleza. 10 Shamba limeharibika, nchi inaomboleza; maana nafaka imeharibika, divai mpya imekauka, mafuta yamepunguka. 11 Tahayarini, enyi wakulima; Pigeni yowe, enyi watunzaji wa mizabibu; Kwa ajili ya ngano na shayiri, Maana mavuno ya mashamba yamepotea. 12 Mzabibu umesinyaa, mtini nao umevia; Nao mkomamanga na mtende na mtofaa; Naam, miti yote ya mashamba imekauka; Maana furaha imekauka katika wanadamu. 13 Jikazeni mkaomboleze, enyi makuhani; Pigeni yowe, enyi wahudumu wa madhabahu; Njoni mlale usiku kucha katika magunia, Enyi wahudumu wa Mungu wangu; Kwa kuwa sadaka ya unga na sadaka ya kinywaji Zimezuiwa katika nyumba ya Mungu wenu. 14 Takaseni saumu, iteni kusanyiko la dini, Wazee na wakusanye wenyeji wote wa nchi; Waende nyumbani kwa Bwana, Mungu wenu, Na kumlilia Bwana, 15 Ole wake siku hii! Kwa maana siku ya Bwana inakaribia, nayo itakuja kama uangamivu utokao kwake aliye Mwenyezi. 16 Je! Chakula hakikukatiliwa mbali mbele ya macho yetu? Naam, furaha na kicheko mbali na nyumba ya Mungu wetu? 17 Mbegu zinaoza chini ya udongo wake; ghala zimeachwa ukiwa; mabanda yamevunjika; kwa maana nafaka imekauka. 18 Jinsi wanyama wanavyougua! Makundi ya ng'ombe yamefadhaika, kwa sababu hawana malisho; naam, makundi ya kondoo yamepata mateso. 19 Ee Bwana, nakulilia wewe; Kwa maana moto umeyala malisho ya nyikani, Na miali ya moto imeteketeza miti yote ya mashamba. 20 Naam, wanyama wa mashamba wanakutwetea wewe; Kwa maana vijito vya maji vimekauka, Na moto umeyateketeza malisho ya nyikani.

Yoeli 2

1 Pigeni tarumbeta katika Sayuni, Pigeni na kelele katika mlima wangu mtakatifu; Wenyeji wote wa nchi na watetemeke; Kwa maana siku ya Bwana inakuja. Kwa sababu inakaribia; 2 siku ya giza na weusi, siku ya mawingu na giza kuu. Kama mapambazuko yakitandazwa juu ya milima, hao ni wakuu, tena wenye nguvu, mfano wao haukuwako kamwe, wala hautakuwako baada ya hao, hata katika miaka ya vizazi vingi. 3 Moto unakula mbele yao; na nyuma yao miali ya moto inateketeza; hiyo nchi inafanana na bustani ya Adeni mbele yao, na nyuma yao imekuwa jangwa tupu; naam, hakuna aliyeokoka asipatikane nao. 4 Kuonekana kwao ni kama kuonekana kwa farasi; na kama wapanda farasi ndivyo wanavyopiga mbio. 5 Kama mshindo wa magari ya vita juu ya vilele vya milima, ndivyo warukavyo; kama mshindo wa miali ya moto ilapo mabua makavu, kama mashujaa waliopangwa tayari kwa vita. 6 Mbele yao watu wanahangaika; nyuso zote zimegeuka kuwa nyeupe kwa hofu. 7 Hupiga mbio kama mashujaa; huupanda ukuta kama watu wa vita; nao huendelea mbele kila mmoja katika njia zake, wala hawapotoshi safu zao. 8 Wala hapana mmoja amsukumaye mwenzake; huendelea mbele kila mmoja katika njia yake; hujifanyizia njia kwa nguvu kati ya silaha, wala hawaachi kuifuata njia yao. 9 Huurukia mji; hupiga mbio juu ya ukuta; hupanda na kuingia ndani ya nyumba; huingia madirishani kama aingiavyo mwivi. 10 Nchi inatetemeka mbele yao; mbingu zinatetemeka; jua na mwezi hutiwa giza, na nyota huacha kuangaza; 11 naye Bwana anatoa sauti yake mbele ya jeshi lake; maana matuo yake ni makubwa sana; kwa maana yeye ni hodari atekelezaye neno lake; kwa kuwa siku ya Bwana ni kuu, yenye kitisho sana; naye ni nani awezaye kuistahimili? 12 Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea; 13 rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya. 14 N'nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia baraka nyuma yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa Bwana, Mungu wenu? 15 Pigeni tarumbeta katika Sayuni, Takaseni saumu, kusanyeni kusanyiko kuu; 16 Kusanyeni watu, litakaseni kusanyiko, Kusanyeni wazee, kusanyeni watoto, Na hao wanyonyao maziwa; Bwana arusi na atoke chumbani mwake, Na bibi arusi katika hema yake. 17 Hao makuhani, wahudumu wa Bwana, na walie Kati ya patakatifu na madhabahu, Na waseme, Uwaachilie watu wako, Ee Bwana, Wala usiutoe urithi wako upate aibu, Hata mataifa watawale juu yao; Kwani waseme kati ya watu, Yuko wapi Mungu wao? 18 Hapo ndipo Bwana alipoona wivu kwa ajili ya nchi yake, akawahurumia watu wake. 19 Bwana akajibu, akawaambia watu wake; Tazameni, nitawaletea nafaka, na divai, na mafuta, nanyi mtashiba kwa vitu hivyo; wala sitawafanya tena kuwa aibu kati ya mataifa; 20 lakini jeshi lililotoka kaskazini nitaliondolea mbali nanyi, nami nitalifukuza mpaka nchi ya ukame na ukiwa; sehemu yake iliyo mbele itaingia katika bahari ya mashariki, na sehemu yake iliyo nyuma itaingia katika bahari ya magharibi; na uvundo wake utapanda juu, na harufu yake mbaya itapanda juu, kwa sababu ametenda mambo makubwa. 21 Ee nchi, usiogope; furahi na kushangilia; kwa kuwa Bwana ametenda mambo makuu. 22 Msiogope, enyi wanyama wa kondeni; maana malisho ya jangwani yanatoa miche, na huo mti unazaa matunda yake, mtini na mzabibu inatoa nguvu zake. 23 Furahini, basi, enyi wana wa Sayuni, mkamfurahie Bwana, Mungu wenu; kwa kuwa yeye huwapa ninyi mvua ya masika, kwa kipimo cha haki, naye huwanyeshea mvua, mvua ya masika, na mvua ya vuli, kama kwanza. 24 Na sakafu za kupepetea zitajaa ngano, na mashinikizo yatafurika kwa divai na mafuta. 25 Nami nitawarudishia hiyo miaka iliyoliwa na nzige, na parare, na madumadu, na tunutu, jeshi langu kubwa nililotuma kati yenu. 26 Nanyi mtakula chakula tele na kushiba, na kulihimidi jina la Bwana, Mungu wenu, aliyewatendea mambo ya ajabu; na watu wangu hawatatahayari kamwe. 27 Nanyi mtajua ya kuwa mimi ni katikati ya Israeli, na ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, wala hakuna mwingine; na watu wangu hawatatahayari kamwe. 28 Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono; 29 tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu. 30 Nami nitaonyesha mambo ya ajabu katika mbingu na katika dunia, damu, na moto, na minara ya moshi. 31 Jua litageuzwa kuwa giza, na mwezi kuwa damu, kabla haijaja hiyo siku ya Bwana iliyo kuu na itishayo. 32 Na itakuwa ya kwamba mtu awaye yote atakayeliita jina la Bwana ataponywa; kwa kuwa katika mlima Sayuni na katika Yerusalemu watakuwako watu watakaookoka, kama Bwana alivyosema; na katika mabaki, hao awaitao Bwana.

Yoeli 3

1 Kwa maana, angalieni, siku zile, na wakati ule, nitakapowarudisha mateka wa Yuda na Yerusalemu, 2 nitakusanya mataifa yote, nami nitawaleta chini katika bonde la Yehoshafau, na huko nitawahukumu kwa ajili ya watu wangu, na kwa ajili ya urithi wangu, Israeli, ambao wamewatawanya kati ya mataifa, na kuigawanya nchi yangu. 3 Nao wamewapigia kura watu wangu; na mtoto mwanamume wamemtoa ili kupata kahaba, na mtoto mwanamke wamemwuza ili kupata divai, wapate kunywa. 4 Naam, na ninyi ni kitu gani kwangu, enyi Tiro, na Sidoni, na nchi zote za Filisti? Je! Mtanirudishia malipo? Au mtanitenda neno lo lote? Upesi na kwa haraka nitawarudishia malipo yenu juu ya vichwa vyenu wenyewe. 5 Kwa kuwa mmetwaa fedha yangu na dhahabu yangu, nanyi mmevichukua vitu vyangu vyema vipendezavyo, na kuviingiza katika hekalu zenu; 6 tena watoto wa Yuda na watoto wa Yerusalemu mmewauzia Wayunani, mpate kuwahamisha mbali na mipaka yao; 7 tazameni, nitawaamsha wapatoke mahali mlipowauza, nami nitawarudishia malipo yenu juu ya vichwa vyenu wenyewe. 8 Na mimi nitawauza wana wenu na binti zenu, na kuwatia katika mikono ya wana wa Yuda, nao watawauzia watu wa Sheba, taifa lililo mbali kabisa; kwa maana Bwana ndiye aliyesema neno hili. 9 Tangazeni haya kati ya mataifa; takaseni vita; waamsheni mashujaa; watu wa vita na wakaribie; na wapande juu. 10 Yafueni majembe yenu yawe panga, na miundu yenu iwe mikuki; aliye dhaifu na aseme, Mimi ni hodari. 11 Fanyeni haraka, mje, enyi mataifa yote, wa pande zote, jikusanyeni pamoja; na huko watelemshe mashujaa wako wote, Ee Bwana. 12 Mataifa na wajihimize, wakapande juu katika bonde la Yehoshafau; maana huko ndiko nitakakoketi niwahukumu mataifa yote yaliyo pande zote. 13 Haya! Utieni mundu, maana mavuno yameiva; njoni, kanyageni; kwa maana shinikizo limejaa, mapipa nayo yanafurika; kwani uovu wao ni mwingi sana. 14 Makutano makubwa, makutano makubwa, wamo katika bonde la kukata maneno! Kwa maana siku ya Bwana i karibu, katika bonde la kukata maneno. 15 Jua na mwezi vimetiwa giza, na nyota zimeacha kuangaza. 16 Naye Bwana atanguruma toka Sayuni, atatoa sauti yake toka Yerusalemu; na mbingu na nchi zitatetemeka; lakini Bwana atakuwa kimbilio la watu wake, na ngome ya wana wa Israeli. 17 Hivyo ndivyo mtakavyojua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu, nikaaye Sayuni, mlima wangu mtakatifu; ndipo Yerusalemu utakapokuwa mtakatifu, wala wageni hawatapita tena ndani yake kamwe. 18 Tena itakuwa siku ile, ya kwamba milima itadondoza divai tamu, na vilima vitatiririka maziwa, na vijito vyote vya Yuda vitatoa maji tele; na chemchemi itatokea katika nyumba ya Bwana, na kulinywesha bonde la Shitimu. 19 Misri itakuwa ukiwa, na Edomu itakuwa jangwa tupu, kwa sababu ya dhuluma waliowatenda wana wa Yuda; kwa sababu wamemwaga damu isiyo na hatia katika nchi yao. 20 Bali Yuda atadumu milele, na Yerusalemu tangu kizazi hata kizazi. 21 Nami nitaitakasa damu yao ambayo sijaitakasa; kwa maana Bwana ndiye akaaye Sayuni.

Amosi 1

1 Maneno ya Amosii, aliyekuwa mmoja wa wachungaji wa Tekoa; maono aliyoyaona katika habari za Israeli, siku za Uzia, mfalme wa Yuda, na siku za Yeroboamu, mwana wa Yoashi, mfalme wa Israeli, miaka miwili kabla ya tetemeko la nchi. 2 Naye alisema, Bwana atanguruma toka Sayuni, Atatoa sauti yake toka Yerusalemu; Na malisho ya wachungaji yataomboleza, Na kilele cha Karmeli kitanyauka. 3 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Dameski, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu wameipura Gileadi kwa vyombo vya kupuria vya chuma; 4 lakini nitapeleka moto uingie katika nyumba ya Hazaeli, nao utayateketeza majumba ya Ben-hadadi. 5 Nami nitalivunja komeo la Dameski, na kuwakatilia mbali wenyeji wa bondeni mwa Aveni, na yeye aishikaye fimbo ya enzi katika Beth-Adini; na watu wa Shamu watakwenda hali ya kufungwa hata Kiri, asema Bwana. 6 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Gaza, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu waliichukua katika hali ya kufungwa kabila nzima, wawatie katika mikono ya Edomu; 7 lakini nitapeleka moto juu ya ukuta wa Gaza, nao utayateketeza majumba yake. 8 Nami nitamkatilia mbali mwenyeji katika Ashdodi; na yeye aishikaye fimbo ya enzi katika Ashkeloni; nami nitaugeuza mkono wangu uwe juu ya Ekroni; na mabaki ya Wafilisti wataangamia, asema Bwana MUNGU. 9 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Tiro, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu wameitia kabila nzima katika mikono ya Edomu, wala hawakulikumbuka agano la udugu; 10 lakini nitapeleka moto juu ya ukuta wa Tiro, nao utayateketeza majumba yake. 11 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Edomu, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu alimfuatia ndugu yake kwa upanga, akatupilia mbali huruma zake zote; hasira yake ikararua-rarua daima, akaishika ghadhabu yake milele; 12 lakini nitapeleka moto juu ya Temani, nao utayateketeza majumba ya Bosra. 13 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya wana wa Amoni, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu wamewapasua wanawake wa Gileadi wenye mimba, ili wapate kuongeza mipaka yao; 14 lakini nitawasha moto katika ukuta wa Raba, nao utayateketeza majumba yake; pamoja na kupiga kelele siku ya vita, pamoja na tufani katika siku ya chamchela; 15 na mfalme wao atakwenda utumwani, yeye na wakuu wake wote pamoja, asema Bwana.

Amosi 2

1 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Moabu, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu aliichoma moto mifupa ya mfalme wa Edomu hata ikawa chokaa; 2 lakini nitapeleka moto juu ya Moabu, nao utayateketeza majumba ya Keriothi; na Moabu atakufa pamoja na mshindo, na kelele, na sauti ya tarumbeta; 3 nami nitamkatilia mbali mwamuzi atoke kati yake, nami nitawaua wakuu wake pamoja naye, asema Bwana. 4 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Yuda, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu wameikataa sheria ya Bwana; wala hawakuzishika amri zake; na maneno yao ya uongo yamewakosesha, ambayo baba zao waliyafuata; 5 lakini nitapeleka moto juu ya Yuda, nao utayateketeza majumba ya Yerusalemu. 6 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Israeli, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu wamewauza wenye haki kwa fedha, na maskini kwa jozi ya viatu; 7 nao hutwetea mavumbi yaliyo juu ya vichwa vya maskini, na kuipotosha njia ya mwenye upole; na mtu na baba yake humwendea mwanamke mmoja, hata kulitia unajisi jina langu takatifu; 8 nao hujilaza karibu na kila madhabahu juu ya nguo zilizowekwa rehani, na katika nyumba ya Mungu wao hunywa divai ya watu waliotozwa fedha. 9 Lakini nalimwangamiza Mwamori mbele yao, ambaye urefu wake ulikuwa kama urefu wa mierezi, tena alikuwa na nguvu kama mialoni; lakini naliyaangamiza matunda yake toka juu, na mizizi yake toka chini. 10 Pia naliwapandisha ninyi kutoka nchi ya Misri, nikawaongoza muda wa miaka arobaini jangwani, ili mpate kuimiliki nchi ya Mwamori. 11 Nami nikawainua watu miongoni mwa wana wenu wawe manabii, na katika vijana wenu wawe Wanadhiri; je! Sivyo hivyo, enyi wana wa Israeli? Asema Bwana. 12 Lakini mliwapa Wanadhiri mvinyo wanywe; mkawaamuru manabii, mkisema, Msifanye unabii. 13 Tazameni, nitawalemea ninyi, Kama gari lilemeavyo lililojaa miganda. 14 Naye apigaye mbio atapotewa na kimbilio; Wala aliye hodari hataongeza nguvu zake; Wala shujaa hatajiokoa nafsi yake; 15 Wala apindaye upinde hatasimama; Wala aliye mwepesi wa miguu hataokoka; Wala apandaye farasi hatajiokoa nafsi yake; 16 Naye mwenye moyo mkuu miongoni mwa mashujaa Atakimbia uchi siku ile, asema Bwana.

Amosi 3

1 Lisikieni neno hili alilolisema Bwana juu yenu, enyi wana wa Israeli, juu ya jamaa yote niliowapandisha kutoka nchi ya Misri, nikisema, 2 Ni ninyi tu niliowajua katika jamaa zote zilizo duniani; kwa sababu hiyo nitawapatiliza ninyi maovu yenu yote. 3 Je! Watu wawili waweza kutembea pamoja, wasipokuwa wamepatana? 4 Je! Simba atanguruma mwituni, asipokuwa na mawindo? Mwana-simba atalia pangoni mwake, ikiwa hakupata kitu? 5 Je! Ndege ataanguka mtegoni juu ya nchi, mahali asipotegewa tanzi? Mtego utafyatuka juu ya nchi, bila kunasa kitu cho chote? 6 Je! Tarumbeta itapigwa mjini, watu wasiogope? Mji utapatikana na hali mbaya, asiyoileta Bwana? 7 Hakika Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake. 8 Simba amekwisha kunguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana MUNGU amenena, ni nani awezaye neno ila kutabiri? 9 Tangazeni habari katika majumba ya Ashdodi, na katika majumba ya nchi ya Misri, mkaseme, Kusanyikeni juu ya milima ya Samaria, katazameni, ni mishindo mikubwa kama nini iliyomo humo, na udhalimu mwingi kama nini uliomo ndani yake. 10 Kwa maana hawajui kutenda haki, asema Bwana, hao wawekao akiba ya jeuri na unyang'anyi katika majumba yao. 11 Basi, haya ndiyo asemayo Bwana MUNGU; Atakuwako adui, kuizunguka nchi pande zote; naye atazishusha chini nguvu zako zikutoke; na majumba yako yatatekwa nyara. 12 Haya ndiyo asemayo Bwana; Kama vile mchungaji apokonyavyo kinywani mwa simba miguu miwili, au kipande cha sikio; ndivyo watakavyopokonywa wana wa Israeli, wakaao Samaria katika pembe ya semadari, na juu ya mito ya hariri ya kitanda. 13 Sikieni, mkashuhudu juu ya nyumba ya Yakobo, asema Bwana, MUNGU wa majeshi. 14 Kwani katika siku ile nitakapompatiliza Israeli makosa yake, nitazipatiliza pia madhabahu za Betheli, na pembe za madhabahu zitakatiliwa mbali, na kuanguka chini. 15 Nami nitaipiga nyumba ya wakati wa baridi pamoja na nyumba ya wakati wa hari; na hizo nyumba za pembe zitaangamia, nazo nyumba kubwa zitakuwa na mwisho, asema Bwana.

Amosi 4

1 Lisikieni neno hili, enyi ng'ombe wa Bashani, mnaokaa juu ya mlima wa Samaria, mnaowaonea maskini, na kuwaponda wahitaji; mnaowaambia bwana zao, Haya! Leteni, tunywe. 2 Bwana MUNGU ameapa kwa utakatifu wake, ya kuwa, tazama, siku zitawajilia, watakapowaondoa ninyi kwa kulabu, na mabaki yenu kwa ndoana. 3 Nanyi mtatoka kwenye mahali palipobomolewa, kila mwanamke moja kwa moja mbele yake; nanyi mtajitupa katika Harmoni, asema Bwana. 4 Njoni Betheli, mkakose; njoni Gilgali, mkaongeze makosa; kaleteni dhabihu zenu kila asubuhi, na zaka zenu kila siku ya tatu; 5 mkachome sadaka ya shukrani, ya kitu kilichotiwa chachu; mkatangaze sadaka mtoazo kwa hiari na kuzihubiri habari zake; kwa maana ndivyo viwapendezavyo ninyi, enyi wana wa Israeli, asema Bwana MUNGU. 6 Mimi nami nimewapa usafi wa meno katika miji yenu yote, na kutindikiwa na mkate mahali penu pote; lakini hamkunirudia mimi, asema Bwana. 7 Tena nimeizuia mvua msiipate, ilipobaki miezi mitatu kabla ya mavuno; nami nimenyesha mvua juu ya mji mmoja, nikaizuia mvua isinyeshe juu ya mji mwingine; sehemu moja ilipata mvua, na sehemu isiyopata mvua ilikatika. 8 Basi kutoka miji miwili mitatu walitanga-tanga kuendea mji mwingine wapate kunywa maji, wasipate ya kuwatosha; lakini hamkunirudia mimi, asema Bwana. 9 Nami nimewapiga kwa ukavu na koga; wingi wa bustani zenu na mashamba yenu ya mizabibu, na mitini yenu na mizeituni yenu imeliwa na tunutu; Lakini hamkunirudia mimi, asema Bwana. 10 Nimewapelekea tauni, kama tauni ya Misri; vijana wenu nimewaua kwa upanga, na farasi wenu nimewachukulia mbali; nami nimeupandisha uvundo wa matuo yenu na kuuingiza katika mianzi ya pua zenu; lakini hamkunirudia mimi, asema Bwana. 11 Baadhi yenu nimewaangamiza, kama hapo Mungu alipoiangamiza Sodoma na Gomora, nanyi mkawa kama kinga kilichonyakuliwa motoni; lakini hamkunirudia mimi, asema Bwana. 12 Basi nitakutenda hivi, Ee Israeli, na kwa sababu nitakutenda hivi, ujiweke tayari kuonana na Mungu wako, Ee Israeli. 13 Kwa maana, angalia, yeye aifanyizaye milima, na kuuumba upepo, na kumwambia mwanadamu mawazo yake, afanyaye asubuhi kuwa giza, na kupakanyaga mahali pa dunia palipoinuka; Bwana, Mungu wa majeshi, ndilo jina lake.

Amosi 5

1 Lisikieni neno hili nilitamkalo liwe maombolezo juu yenu, enyi nyumba ya Israeli. 2 Bikira wa Israeli ameanguka; hatainuka tena; Ameangushwa katika nchi yake; hakuna mtu wa kumwinua. 3 Kwa kuwa Bwana MUNGU asema hivi; Mji uliotoka nje wenye watu elfu, utasaziwa watu mia, na mji uliotoka wenye watu mia, utasaziwa watu kumi, kwa nyumba ya Israeli. 4 Maana Bwana awaambia hivi nyumba ya Israeli, Nitafuteni mimi, nanyi mtaishi; 5 bali msitafute Betheli, wala msiingie Gilgali, wala msipite kwenda Beer-sheba; kwani Gilgali hakika yake itakwenda utumwani, na Betheli itakuwa ubatili. 6 Mtafuteni Bwana, nanyi mtaishi; asije akawaka kama moto katika nyumba ya Yusufu, nao ukateketeza, asiwepo mtu awezaye kuuzima katika Betheli. 7 Ninyi mnaogeuza hukumu kuwa uchungu, na kuiangusha haki chini, 8 mtafuteni yeye afanyaye Kilimia na Orioni, na kukigeuza kivuli cha mauti kuwa asubuhi, na kuufanya mchana kuwa giza kwa usiku; yeye ayaitaye maji ya bahari, na kuyamwaga juu ya uso wa nchi; Bwana, ndilo jina lake; 9 yeye aletaye uharibifu wa ghafula juu yao walio hodari, hata uharibifu uipate ngome. 10 Wao humchukia yeye akemeaye langoni, nao humzira anenaye maneno ya adili. 11 Basi, kwa kuwa mnamkanyaga maskini, na kumtoza ngano; ninyi mmejenga nyumba za mawe yaliyochongwa, lakini hamtakaa ndani yake; ninyi mmepanda mashamba mazuri ya mizabibu, lakini hamtakunywa divai yake. 12 Maana mimi najua jinsi maasi yenu yalivyo mengi, na jinsi dhambi zenu zilivyo kubwa; ninyi mnaowaonea wenye haki, mnaopokea rushwa, na kuwageuza wahitaji langoni wasipate haki yao. 13 Kwa ajili ya hayo mwenye busara atanyamaza kimya wakati kama huo; kwa kuwa ni wakati mbaya. 14 Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi; hivyo Bwana, Mungu wa majeshi, atakuwa pamoja nanyi, kama msemavyo. 15 Yachukieni mabaya; yapendeni mema; mkaithibitishe haki langoni; yamkini kwamba Bwana, Mungu wa majeshi, atawafanyia fadhili mabaki ya Yusufu. 16 Kwa ajili ya hayo, asema Bwana, Mungu wa majeshi, aliye Bwana; Kutakuwako maombolezo katika njia kuu zote; nao watasema katika njia zote, Ole! Ole! Nao watamwita mkulima aje kuombolea, na hao walio hodari wa kulia waje kuomboleza. 17 Tena katika mashamba yote ya mizabibu kutakuwako kulia; kwa maana mimi nitapita katikati yako, asema Bwana. 18 Ole wenu! Ninyi mnaoitamani siku ya Bwana; kwani kuitamani siku ya Bwana? Ni giza, wala si nuru. 19 Ni kama mtu aliyemkimbia simba, akakutana na dubu; au aliingia katika nyumba akauegemeza mkono wake ukutani, nyoka akamwuma. 20 Je! Siku ya Bwana haitakuwa giza, wala si nuru? Naam, yenye giza sana, wala haina mwanga. 21 Mimi nazichukia sikukuu zenu, nazidharau, nami sitapendezwa na makutano yenu ya dini. 22 Naam, ijapokuwa mnanitolea sadaka zenu za kuteketezwa na sadaka zenu za unga, sitazikubali; wala sitaziangalia sadaka zenu za amani, na za wanyama walionona. 23 Niondoleeni kelele za nyimbo zenu; kwa maana sitaki kuzisikia sauti za vinanda vyenu. 24 Lakini hukumu na itelemke kama maji, na haki kama maji makuu. 25 Je! Mliniletea dhabihu na sadaka jangwani muda wa miaka arobaini, enyi nyumba ya Israeli? 26 Naam, mtamchukua Sikuthi, mfalme wenu, na Kiuni, sanamu zenu, nyota ya mungu wenu, mliojifanyizia wenyewe. 27 Kwa sababu hiyo nitawahamisha, hali ya kufungwa, mwende mbali kupita Dameski, asema Bwana, ambaye jina lake ni Mungu wa majeshi.

Amosi 6

1 Ole wao wanaostarehe katika Sayuni, na hao wanaokaa salama katika mlima wa Samaria, watu mashuhuri wa taifa lililo la kwanza, ambao nyumba ya Israeli huwaendea. 2 Piteni hata Kalne, mkaone; tena tokea huko enendeni hata Hamathi iliyo kuu; kisha shukeni hata Gathi ya Wafilisti; je! Ninyi ni bora kuliko falme hizi? Au mpaka wao ni mkubwa kuliko mpaka wenu? 3 Ninyi mnaoiweka mbali siku hiyo mbaya, na kulileta karibu kao la udhalimu; 4 ninyi mnaolala juu ya vitanda vya pembe, na kujinyosha juu ya masemadari yenu; ninyi mnaokula wana-kondoo wa kundi, na ndama waliomo zizini; 5 ninyi mnaoimba nyimbo za upuzi pamoja na sauti ya vinanda, na kujifanyizia vinanda vya namna nyingi, kama vile Daudi; 6 ninyi mnaokunywa divai katika mabakuli, na kujipaka marhamu iliyo nzuri; lakini hawahuzuniki kwa sababu ya mateso ya Yusufu. 7 Basi kwa ajili ya hayo sasa watakwenda utumwani pamoja na wa kwanza watakaokwenda utumwani, na kelele za machezo za hao waliojinyosha zitakoma. 8 Bwana MUNGU ameapa kwa nafsi yake, asema Bwana, Mungu wa majeshi; Naizira fahari ya Yakobo, nachukizwa na majumba yake; kwa sababu hiyo nitautoa huo mji, pamoja na wote waliomo ndani yake. 9 Hata itakuwa, wakisalia wanaume kumi katika nyumba moja, watakufa. 10 Na mjomba wa mtu atakapomwinua, yaani, yeye amchomaye moto, ili atoe mifupa yake nyumbani, naye atakapomwambia yeye aliye katika pande za ndani za nyumba, Je! Yuko mtu ye yote pamoja nawe? Naye atakaposema, La, hapana; ndipo atasema, Nyamaza kimya; maana hatuna ruhusa kulitaja jina la Bwana. 11 Kwa maana, angalia, Bwana atoa amri, na nyumba kubwa itapigwa na kuwa na mahali palipobomolewa, na nyumba ndogo nayo itapigwa iwe na nyufa. 12 Je! Farasi watapiga mbio juu ya mwamba? Je! Mtu atalima na ng'ombe huko? Hata mmegeuza hukumu kuwa uchungu, na matunda ya haki kuwa pakanga; 13 ninyi mnaolifurahia jambo lisilo na maana, msemao, Je! Hatukujipatia pembe kwa nguvu zetu wenyewe? 14 Maana, angalia, nitaondokesha taifa juu yenu, enyi nyumba ya Israeli, asema Bwana, Mungu wa majeshi, nao watawatesa ninyi toka mahali pa kuingilia katika Hamathi hata kijito cha Araba.

Amosi 7

1 Haya ndiyo aliyonionyesha Bwana MUNGU; tazama, aliumba nzige mwanzo wa kuchipuka kwake mimea wakati wa vuli; na tazama, ilikuwa mimea ya wakati wa vuli baada ya mavuno ya mfalme. 2 Ikawa, nzige walipokwisha kula majani ya nchi, ndipo nikasema, Ee Bwana MUNGU, samehe, nakusihi; Yakobo atasimamaje? Kwa maana ni mdogo. 3 Bwana akaghairi katika jambo hili. Jambo hili halitakuwa, asema Bwana. 4 Haya ndiyo aliyonionyesha Bwana MUNGU; tazama, Bwana MUNGU aliita ili kushindana kwa moto; nao ukavila vilindi vikuu, ukataka kuiteketeza nchi kavu. 5 Ndipo nikasema, Ee Bwana MUNGU, acha, nakusihi; Yakobo atasimamaje? Kwa maana ni mdogo. 6 Bwana akaghairi katika jambo hili pia. Jambo hili halitakuwa, asema Bwana MUNGU. 7 Haya ndiyo aliyonionyesha; na tazama, Bwana alisimama karibu na ukuta uliojengwa kwa timazi, mwenye timazi mkononi mwake. 8 Bwana akaniambia, Amosii, unaona nini? Nikasema, Naona timazi. Ndipo Bwana akasema, Tazama, nitaweka timazi kati ya watu wangu Israeli; sitawapita tena kamwe; 9 na mahali palipoinuka pa Isaka patakuwa ukiwa, na mahali patakatifu pa Israeli pataharibika; nami nitaondoka nishindane na nyumba ya Yeroboamu kwa upanga. 10 Ndipo Amazia, kuhani wa Betheli, akapeleka habari kwa Yeroboamu, mfalme wa Israeli, akisema, Amosii amefanya fitina juu yako kati ya nyumba ya Israeli; nchi haiwezi kustahimili maneno yake yote. 11 Kwa maana Amosii asema hivi, Yeroboamu atakufa kwa upanga, na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali, hali ya kufungwa, atoke katika nchi yake. 12 Tena Amazia akamwambia Amosii, Ewe mwonaji, nenda zako, ikimbilie nchi ya Yuda, ukale mkate huko, ukatabiri huko; 13 lakini usitabiri tena huku Betheli; kwa maana ni mahali patakatifu pa mfalme, nayo ni nyumba ya kifalme. 14 Ndipo Amosii akajibu akamwambia Amazia, Mimi sikuwa nabii, wala sikuwa mwana wa nabii; bali nalikuwa mchungaji, na mtunza mikuyu; 15 naye Bwana akanitwaa, katika kufuatana na kundi; Bwana akaniambia, Enenda uwatabirie watu wangu Israeli. 16 Basi, sasa lisikie neno la Bwana; Wewe unasema, Usitabiri juu ya Israeli, wala usitoe neno lako juu ya nyumba ya Isaka; 17 kwa hiyo, Bwana asema hivi, Mke wako atakuwa kahaba mjini, na wana wako na binti zako wataanguka kwa upanga, na shamba lako litagawanywa kwa kamba; na wewe mwenyewe utakufa katika nchi iliyo najisi; na bila shaka Israeli atachukuliwa mbali hali ya kufungwa kutoka nchi yake.

Amosi 8

1 Haya ndiyo aliyonionyesha Bwana MUNGU; tazama, kikapu cha matunda ya wakati wa hari. 2 Akaniambia, Amosii, unaona nini? Nikasema, Naona kikapu cha matunda ya wakati wa hari. Ndipo Bwana akaniambia, Mwisho wao umewajilia watu wangu Israeli; sitawapita tena kamwe. 3 Tena nyimbo za hekaluni zitakuwa vilio siku ile, asema Bwana MUNGU; mizoga itakuwa mingi; kila mahali wataitupa, wakinyamaza kimya. 4 Lisikieni hili, ninyi mnaopenda kuwameza wahitaji, na kuwakomesha maskini wa nchi, 5 mkisema, Mwezi mpya utaondoka lini, tupate kuuza nafaka? Na sabato nayo, tupate kuandika ngano? Mkiipunguza efa na kuiongeza shekeli, mkidanganya watu kwa mizani ya udanganyifu; 6 tupate kuwanunua maskini kwa fedha, na wahitaji kwa jozi ya viatu; na kuziuza takataka za ngano. 7 Bwana ameapa kwa fahari ya Yakobo, Hakika sitazisahau kamwe kazi zao hata mojawapo. 8 Kwa ajili ya hayo, je! Haitatetemeka nchi, na kuomboleza kila mtu akaaye ndani yake? Naam, itainuka yote pia kama huo Mto; nayo itataabika na kupwa tena kama Mto wa Misri. 9 Tena itakuwa siku hiyo, asema Bwana MUNGU, nitalifanya jua litue wakati wa adhuhuri, nami nitaitia nchi giza wakati wa nuru ya mchana. 10 Nami nitazigeuza sikukuu zenu kuwa maombolezo, na nyimbo zenu zote kuwa vilio; nami nitatia nguo za magunia katika viuno vyote, na upaa katika kila kichwa; nami nitayafanya haya kuwa kama maombolezo kwa ajili ya mwana wa pekee, na mwisho wake kama siku ya uchungu. 11 Angalia, siku zinakuja, asema Bwana MUNGU, ambazo nitaleta njaa katika nchi; si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya Bwana. 12 Nao watatanga-tanga toka bahari hata bahari; na toka upande wa kaskazi hata upande wa mashariki; watapiga mbio, wakienda huko na huko, kulitafuta neno la Bwana, wasilione. 13 Siku hiyo wanawali wazuri na wavulana watazimia kwa kiu. 14 Na hao waapao kwa dhambi ya Samaria, na kusema, Kama aishivyo Mungu wako, Ee Dani, na, Kama iishivyo njia ya Beer-sheba, hao nao wataanguka, wasiinuke tena.

Amosi 9

1 Nalimwona Bwana akisimama karibu na madhabahu; akasema, vipigo vichwa vya nguzo, hata vizingiti vitikisike; vivunje vipande vipande juu ya kichwa cha kila mmoja wao; nami nitamwua mtu wa mwisho wao kwa upanga; hapana hata mmoja wao atakayekimbia, wala hataokoka hata mmoja wao. 2 Wajapochimba waingie katika kuzimu, mkono wangu utawatoa huko; nao wajapopanda hata mbinguni, nitawatelemsha toka huko. 3 Nao wajapojificha katika kilele cha Karmeli, nitawatafuta na kuwatoa toka huko; na wajapositirika katika vilindi vya bahari nisiwaone, nitamwagiza joka huko, naye atawauma. 4 Nao wajapokwenda hali ya kufungwa mbele ya adui zao, nitauagiza upanga huko, nao utawaua; nami nitawaelekezea macho yangu niwatende mabaya, wala si mema. 5 Kwa maana Bwana, MUNGU wa majeshi, ndiye aigusaye nchi, nayo ikayeyuka, na wote wakaao ndani yake wataomboleza; nayo itainuka yote pia kama Mto, nayo itakupwa tena kama Mto wa Misri. 6 Yeye ndiye avijengaye vyumba vyake mbinguni, na kuweka misingi ya kuba yake juu ya nchi; yeye ndiye ayaitaye maji ya bahari, na kuyamwaga juu ya uso wa nchi; Bwana ndilo jina lake. 7 Je! Ninyi si kama wana wa Wakushi kwangu mimi, enyi wana wa Israeli, asema Bwana? Je! Mimi sikuwapandisha Israeli toka nchi ya Misri, na Wafilisti toka Kaftori, na Washami toka Kiri? 8 Angalieni, macho ya Bwana MUNGU yanauangalia ufalme wenye dhambi, nami nitauangamiza utoke juu ya uso wa dunia; lakini sitaiangamiza kabisa nyumba ya Yakobo, asema Bwana. 9 Kwa maana, angalieni, nitatoa amri, nami nitaipepeta nyumba ya Israeli katika mataifa yote, kama vile ngano ipepetwavyo katika ungo lakini hata chembe moja iliyo ndogo haitaanguka chini. 10 Wenye dhambi wote katika watu wangu watakufa kwa upanga, hao wasemao, Mabaya hayatatupata nyuma wala mbele. 11 Siku hiyo nitaiinua tena maskani ya Daudi iliyoanguka, na kuziba mahali palipobomoka; nami nitayainua magofu yake, na kuyajenga kama siku za kale; 12 wapate kuyamiliki mabaki ya Edomu, na mataifa yote yaitwayo kwa jina langu, asema Bwana, afanyaye hayo. 13 Angalieni, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo huyo alimaye atamfikilia avunaye, na yeye akanyagaye zabibu atamfikilia apandaye mbegu; nayo milima itadondoza divai tamu, na vilima vyote vitayeyuka. 14 Nami nitawarejeza tena watu wangu Israeli waliohamishwa, nao wataijenga miji iliyoachwa maganjo, na kukaa ndani yake; nao watapanda mizabibu katika mashamba, na kunywa divai yake; nao watafanyiza bustani, na kula matunda yake. 15 Nami nitawapanda katika nchi yao, wala hawatang'olewa tena watoke katika nchi yao niliyowapa, asema Bwana, Mungu wako.

Obadia 1

1 Maono yake Obadia. Ndivyo asemavyo Bwana MUNGU juu ya Edomu; Tumepata habari kwa Bwana, Na mjumbe ametumwa kati ya mataifa, Akisema,Haya,inukeni ninyi;Na tuinuke tupigane naye. 2 Tazama, nimekufanya mdogo kati ya mataifa; Umedharauliwa sana. 3 Kiburi cha moyo wako kimekudanganya, Wewe ukaaye katika pango za majabali, Mwenye makao yako juu sana; Asemaye moyoni, Ni nani atakayenishusha mimi? 4 Ujapopanda juu kama tai, Ijapokuwa kioto chako kimewekwa kati ya nyota, Nitakushusha kutoka huko; asema Bwana. 5 Kama wevi wangekujilia, kama wanyang'anyi wangekujilia usiku, (jinsi ulivyokatiliwa mbali!) Je! Wasingeiba kiasi cha kuwatosha? Kama wachumao zabibu wangekujilia, je! Wasingeacha baadhi ya zabibu, ziokotwe? 6 Jinsi watu wa Esau wanavyotafutwa-tafutwa! Jinsi hazina zake zilizofichwa zinavyoulizwa-ulizwa! 7 Watu wote wa mapatano yako Wamekufukuza, hata mipakani; Wale waliofanya amani nawe Wamekudanganya, na kukushinda; Walao mkate wako wameweka mtego chini yako; Wala hana ufahamu wa hayo ndani yake. 8 Siku hiyo, je! Sitawaangamiza watu wenye akili katika Edomu, na wenye ufahamu katika kilima cha Esau? Asema Bwana. 9 Na mashujaa wako, Ee Temani, watafadhaika, hata iwe kila mtu akatiliwe mbali kwa kuuawa katika kilima cha Esau. 10 Kwa sababu ya udhalimu aliotendwa ndugu yako Yakobo, aibu itakufunika, nawe utakatiliwa mbali hata milele. 11 Siku ile uliposimama upande, siku ile wageni walipochukua mali zake, na watu wa kabila nyingine walipoingia katika malango yake, na kumpa kura juu ya Yerusalemu, wewe nawe ulikuwa kama mmoja wao. 12 Lakini usiitazame siku ya ndugu yako, siku ya mashaka yake, wala usisimange juu ya wana wa Yuda siku ya kuangamizwa kwao; wala usinene maneno ya kiburi katika siku ya shida yao. 13 Usiingie katika lango la watu wangu, siku ya msiba wao; naam, usiyatazame mateso yao, siku ya msiba wao; wala usitie mikono yako juu ya mali zao, siku ya msiba wao. 14 Wala usisimame penye njia panda, ili kuwakatilia mbali watu wake wakimbiao; wala usiwatoe watu wake waliosalia, katika siku ya dhiki. 15 Kwa maana hiyo siku ya Bwana i karibu juu ya mataifa yote; kama ulivyotenda, ndivyo utakavyotendwa; malipo yako yatakurudia juu ya kichwa chako mwenyewe. 16 Kwa maana kama vile mlivyokunywa juu ya mlima wangu mtakatifu, ndivyo mataifa yote watakavyokunywa daima; naam, watakunywa na kubabaika, nao watakuwa kana kwamba hawakuwa kamwe. 17 Bali katika mlima Sayuni watakuwako wenye kuokoka, nao utakuwa mtakatifu; na nyumba ya Yakobo watamiliki milki zao. 18 Na nyumba ya Yakobo itakuwa moto, na nyumba ya Yusufu itakuwa mwali wa moto, na nyumba ya Esau itakuwa mabua makavu, nao watawaka kati yao, na kuwateketeza; wala hatasalia mtu awaye yote katika nyumba ya Esau; kwa kuwa Bwana amesema hayo. 19 Na watu wa Negebu wataumiliki mlima wa Esau; na watu wa Shefela watawamiliki Wafilisti; nao watalimiliki konde la Efraimu, na konde la Samaria, na Benyamini atamiliki Gileadi. 20 Na watu wa jeshi hili la wana wa Israeli waliotekwa, walio kati ya Wakanaani, watamiliki mpaka Sarepta; na hao watu wa Yerusalemu waliotekwa, waliomo Sefaradi, wataimiliki miji ya Negebu.

Yona 1

1 Basi neno la Bwana lilimjia Yona, mwana wa Amitai, kusema, 2 Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukapige kelele juu yake; kwa maana uovu wao umepanda juu mbele zangu. 3 Lakini Yona akaondoka akimbilie Tarshishi, apate kujiepusha na uso wa Bwana; akatelemka hata Yafa, akaona merikebu inayokwenda Tarshishi; basi, akatoa nauli, akapanda merikebuni, aende pamoja nao Tarshishi, ajiepushe na uso wa Bwana. 4 Lakini Bwana alituma upepo mkuu baharini, ikawa tufani kubwa baharini, hata merikebu ikawa karibu na kuvunjika. 5 Basi wale mabaharia wakaogopa, kila mtu akamwomba mungu wake; nao wakatupa baharini shehena iliyokuwa merikebuni, ili kuupunguza uzito wake. Lakini Yona alikuwa ameshuka hata pande za ndani za merikebu; akajilaza, akapata usingizi. 6 Basi nahodha akamwendea, akamwambia, Una nini, Ewe ulalaye usingizi? Amka, ukamwombe Mungu wako; labda Mungu huyo atatukumbuka, tusipotee. 7 Wakasemezana kila mtu na mwenzake, Haya, na mpige kura, mpate kujua mabaya haya yametupata kwa sababu ya nani. Basi wakapiga kura, nayo kura ikamwangukia Yona. 8 Ndipo wakamwambia, Tafadhali utuambie, wewe ambaye mabaya haya yametupata kwa sababu yako; kazi yako ni kazi gani? Nawe umetoka wapi? Nchi yako ni nchi ipi? Nawe u mtu wa kabila gani? 9 Akawaambia, Mimi ni Mwebrania; nami namcha Bwana, Mungu wa mbingu, aliyeziumba bahari na nchi kavu. 10 Ndipo watu wale wakaogopa mno, wakamwambia, Ni jambo gani hili ulilolitenda! Kwa maana watu wale walijua ya kuwa amekimbia, ajiepushe na uso wa Bwana, kwa sababu alikuwa amewajulisha. 11 Basi wakamwambia, Tukutende nini, ili bahari itulie? Kwa maana bahari ilikuwa inazidi kuchafuka. 12 Naye akawaambia, Nikamateni, mnitupe baharini; basi bahari itatulia; kwa maana najua ya kuwa ni kwa ajili yangu tufani hii imewapata. 13 Lakini wale watu wakavuta makasia kwa nguvu, ili wapate kurudi pwani, wasiweze; kwa maana bahari ilizidi kuwachafukia sana. 14 Basi wakamlilia Bwana, wakasema, Twakuomba, Ee Bwana, twakuomba, tusiangamie kwa ajili ya uhai wa mtu huyu, wala usitupatilize kwa ajili ya damu isiyo na hatia; kwa maana wewe, Bwana, umefanya kama ulivyopenda. 15 Basi wakamkamata Yona, wakamtupa baharini, nayo bahari ikaacha kuchafuka. 16 Ndipo wale watu wakamwogopa Bwana mno, wakamtolea Bwana sadaka, na kuweka nadhiri. 17 Bwana akaweka tayari samaki mkubwa ili ammeze Yona, naye Yona akawa ndani ya tumbo la samaki yule muda wa siku tatu, mchana na usiku.

Yona 2

1 Ndipo Yona akamwomba Bwana, Mungu wake, katika tumbo la yule samaki, 2 Akasema, Nalimlilia Bwana kwa sababu ya shida yangu, Naye akaniitikia; Katika tumbo la kuzimu naliomba, Nawe ukasikia sauti yangu. 3 Maana ulinitupa vilindini, Ndani ya moyo wa bahari; Gharika ya maji ikanizunguka pande zote; Mawimbi yako yote na gharika zako zote zimepita juu yangu. 4 Nami nikasema, Nimetupwa mbali na macho yako; Lakini nitatazama tena kukabili hekalu lako takatifu. 5 Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu; Vilindi vilinizunguka; Mwani ulikizinga kichwa changu; 6 Nalishuka hata pande za chini za milima; Hiyo nchi na mapingo yake yalinifunga hata milele; Lakini umeipandisha nafsi yangu kutoka shimoni, Ee Bwana, Mungu wangu, 7 Roho yangu ilipozimia ndani yangu, Nalimkumbuka Bwana; Maombi yangu yakakuwasilia, Katika hekalu lako takatifu. 8 Watu waangaliao mambo ya ubatili na uongo Hujitenga na rehema zao wenyewe; 9 Lakini mimi nitakutolea sadaka kwa sauti ya shukrani; Nitaziondoa nadhiri zangu. Wokovu hutoka kwa Bwana. 10 Bwana akasema na yule samaki, naye akamtapika Yona pwani.

Yona 3

1 Neno la Bwana likamjia Yona mara ya pili, kusema, 2 Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa; ukaihubiri habari nitakayokuamuru. 3 Basi Yona akaondoka, akaenda Ninawi, kama Bwana alivyonena. Basi Ninawi ulikuwa mji mkubwa mno, ukubwa wake mwendo wa siku tatu. 4 Yona akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa. 5 Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo. 6 Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu. 7 Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya mfalme na wakuu wake; kusema, Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng'ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; 8 bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio mikononi mwake. 9 Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha hasira yake kali, ili msiangamizwe? 10 Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende.

Yona 4

1 Lakini jambo hili lilimchukiza Yona sana, naye akakasirika. 2 Akamwomba Bwana, akasema, Nakuomba, Ee Bwana; sivyo hivyo nilivyosema, hapo nilipokuwa katika nchi yangu? Hii ndiyo sababu nalifanya haraka kukimbilia Tarshishi; kwa maana nalijua ya kuwa wewe u Mungu mwenye neema, umejaa huruma, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema, nawe waghairi mabaya. 3 Basi, sasa, Ee Bwana, nakuomba, uniondolee uhai wangu; maana ni afadhali nife mimi kuliko kuishi. 4 Naye Bwana akasema, Je! Unatenda vema kukasirika? 5 Ndipo Yona akatoka mjini, akaketi upande wa mashariki wa mji, akajifanyia kibanda huko, akakaa chini yake uvulini, hata aone mji ule utakuwaje. 6 Na Bwana Mungu aliweka tayari mtango, akaufanya ukue juu ya Yona, ili uwe kivuli juu ya kichwa chake, na kumponya katika hali yake mbaya. Basi Yona akafurahi sana kwa sababu ya ule mtango. 7 Lakini siku ya pili kulipopambazuka, Mungu akaweka tayari buu, nalo likautafuna ule mtango, ukakatika. 8 Basi ikawa, jua lilipopanda juu, Mungu akaweka tayari upepo wa mashariki, wenye hari nyingi; jua likampiga Yona kichwani, hata akazimia, naye akajitakia kufa, akasema, Ni afadhali nife mimi kuliko kuishi. 9 Mungu akamwambia Yona, Je! Unatenda vema kukasirika kwa ajili ya mtango? Naye akasema, Ndiyo, natenda vema kukasirika hata kufa. 10 Bwana akamwambia, Wewe umeuhurumia mtango, ambao hukuufanyia kazi, wala kuuotesha; uliomea katika usiku mmoja, na kuangamia katika usiku mmoja; 11 na mimi, je! Haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?

Mika 1

1 Hili ndilo neno la Bwana lililomjia Mika, Mmorashti, katika siku za Yothamu, na Ahazi, na Hezekia, wafalme wa Yuda; maono aliyoyaona katika habari za Samaria, na Yerusalemu. 2 Sikilizeni, enyi watu wa kabila zote; sikiliza, Ee dunia, na vyote vilivyomo; Bwana MUNGU na ashuhudie juu yenu, yeye Bwana kutoka hekalu lake takatifu. 3 Kwa maana, angalieni, Bwana anakuja akitoka mahali pake, naye atashuka, na kupakanyaga mahali pa dunia palipoinuka. 4 Na hiyo milima itayeyuka chini yake, nayo mabonde yatapasuliwa, kama vile nta iliyo mbele ya moto, kama maji yaliyomwagika tena kutelemka gengeni. 5 Kwa sababu ya kosa la Yakobo yametokea haya yote, na kwa sababu ya makosa ya nyumba ya Israeli. Nini kosa la Yakobo? Je, silo Samaria? Na nini mahali pa Yuda palipoinuka? Sipo Yerusalemu? 6 Kwa ajili ya hayo nitafanya Samaria kuwa kama chungu katika shamba, na kama miche ya shamba la mizabibu; nami nitayatupa mawe yake bondeni, nami nitaifunua misingi yake. 7 Na sanamu zake zote za kuchonga zitapondwa-pondwa, na ijara zake zote zitateketezwa kwa moto, na sanamu zake zote nitazifanya ukiwa; kwa kuwa amezikusanya kwa ujira wa kahaba, nazo zitaurudia ujira wa kahaba. 8 Kwa ajili ya hayo nitaomboleza na kulia, Nitakwenda nimevua nguo, ni uchi; Nitafanya mlio kama wa mbweha, Na maombolezo kama ya mbuni. 9 Kwa maana jeraha zake haziponyekani; Maana msiba umeijilia hata Yuda, Unalifikia lango la watu wangu, Naam, hata Yerusalemu. 10 Msiyahubiri haya katika Gathi, msilie kamwe; Katika Beth-le-Afra ugae-gae mavumbini. 11 Piteni; uende ukaaye Shafiri, hali ya uchi na aibu; Hivyo akaaye Saanani hajatokea nje; Maombolezo ya Beth-eseli yatawaondolea tegemeo lake; 12 Maana akaaye Marothi ana utungu wa mema; Kwa kuwa msiba umeshuka toka kwa Bwana, Umefika mpaka lango la Yerusalemu. 13 Mfungie gari la vita farasi Aliye mwepesi, ukaaye Lakishi; Alikuwa mwanzo wa dhambi kwa binti Sayuni; Maana makosa ya Israeli yameonekana kwako. 14 Kwa hiyo utaipa Moresheth-Gathi zawadi ya kuagia; Nyumba za Akzibu zitakuwa kijito kidanganyacho wafalme wa Israeli. 15 Bado, ukaaye Maresha, nitakuletea yeye atakayekumiliki; Utukufu wa Israeli utafika mpaka Adulamu. 16 Jifanyie upaa, jikate nywele zako, Kwa ajili ya watoto waliokufurahisha; Panua upaa wako kama tai; Kwa maana wamekwenda mbali nawe utumwani.

Mika 2

1 Ole wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao. 2 Nao hutamani mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na nyumba yake, naam, mtu na urithi wake. 3 Basi Bwana asema hivi, Angalia, nakusudia jambo baya juu ya jamaa hii, ambalo hamtazitoa shingo zenu, wala hamtakwenda kwa kiburi; kwa maana ni wakati mbaya. 4 Siku hiyo watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na kusema, Sisi tumeangamizwa kabisa; Yeye analibadili fungu la watu wangu; Jinsi anavyoniondolea hilo! Awagawia waasi mashamba yetu. 5 Kwa hiyo hutakuwa na mtu atakayeitupa kamba kwa kura katika mkutano wa Bwana. 6 Msitabiri, ndivyo watabirivyo; wasiyatabiri mambo haya; lawama hazikomi. 7 Je! Litasemwa neno hili, enyi nyumba ya Yakobo, Roho ya Bwana imepunguzwa? Je! Haya ni matendo yake? Je! Maneno yangu hayamfai yeye aendaye kwa unyofu? 8 Lakini siku hizi mmeinuka kama adui za watu wangu; mwaipokonya joho iliyo juu ya nguo za hao wapitao salama kama watu wasiopenda vita. 9 Wanawake wa watu wangu mwawatupa nje ya nyumba zao nzuri; watoto wao wachanga mwawanyang'anya utukufu wangu milele. 10 Ondokeni, mwende zenu; maana hapa sipo mahali pa raha yenu; kwa sababu ya uchafu mtaangamizwa, naam, kwa maangamizo mazito sana. 11 Mtu akienda kwa roho ya uongo, akinena maneno ya uongo, akisema, Nitakutabiria habari ya mvinyo na kileo; mtu huyu atakuwa nabii wao watu hawa. 12 Hakika nitakukusanya, Ee Yakobo, nyote pia; Bila shaka nitawakusanya waliobaki wa Israeli; Nitawaweka pamoja kama kondoo wa Bozra; Kama kundi la kondoo kati ya malisho yao; Watafanya mvumo kwa wingi wa watu; 13 Avunjaye amekwea juu mbele yao; Wamebomoa mahali, wakapita mpaka langoni, Wakatoka nje huko; Mfalme wao naye amepita akiwatangulia, Naye Bwana ametangulia mbele yao.

Mika 3

1 Nikasema, Tafadhali sikieni, enyi vichwa vya Yakobo, mnaoitawala nyumba ya Israeli. Je! Haiwapasi ninyi kujua hukumu? 2 Ninyi mnaoyachukia mema, na kuyapenda mabaya; ninyi mnaowachuna watu ngozi yao, na nyama mifupani mwao. 3 Naam, mnakula nyama ya watu wangu, na kuwachuna ngozi zao, na kuivunja mifupa yao; naam, kuwakata vipande vipande kama kwa kutiwa chunguni, na kama nyama sufuriani. 4 Ndipo watakapomwomba Bwana, asiwaitikie; naam, atawaficha uso wake wakati huo, kwa kadiri walivyotenda mabaya kwa matendo yao. 5 Bwana asema hivi katika habari za manabii wanaowakosesha watu wangu; hao waumao kwa meno yao, na kulia, Amani; na mtu awaye yote asiyetia kitu vinywani mwao, wao humwandalia vita. 6 Kwa hiyo itakuwa usiku kwenu, msipate kuona maono; tena itakuwa giza kwenu, msiweze kubashiri; nalo jua litawachwea manabii, nao mchana utakuwa mweusi juu yao. 7 Na hao waonaji watatahayarika, na wenye kubashiri watafadhaika; naam, hao wote watajifunika midomo yao; kwa maana; hapana jawabu la Mungu. 8 Bali mimi, hakika nimejaa nguvu kwa roho ya Bwana; nimejaa hukumu na uwezo; nimhubiri Yakobo kosa lake, na Israeli dhambi yake. 9 Sikieni haya, tafadhali, enyi vichwa vya nyumba ya Yakobo, mnaoitawala nyumba ya Israeli, mnaochukia hukumu, na kuipotosha adili. 10 Wanaijenga Sayuni kwa damu, na Yerusalemu kwa uovu. 11 Wakuu wake huhukumu ili wapate rushwa, na makuhani wake hufundisha ili wapate ijara, na manabii wake hubashiri ili wapate fedha; ila hata hivyo watamtegemea Bwana, na kusema, Je! Hayupo Bwana katikati yetu? Hapana neno baya lo lote litakalotufikia. 12 Basi, kwa ajili yenu, Sayuni utalimwa kama shamba lilimwavyo, na Yerusalemu utakuwa magofu; na mlima wa nyumba utakuwa kama mahali palipoinuka msituni.

Mika 4

1 Lakini itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya Bwana utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi. 2 Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana, na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; kwa maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana litatoka Yerusalemu. 3 Naye atafanya hukumu kati ya watu wa kabila nyingi, naye atawakemea mataifa wenye nguvu walio mbali; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. 4 Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha Bwana wa majeshi kimesema hivi. 5 Kwa maana mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la Bwana, Mungu wetu, milele na milele. 6 Katika siku ile, asema Bwana, nitamkusanya yeye achechemeaye, nami nitamrudisha yeye aliyefukuzwa, na yeye niliyemtesa. 7 Nami nitamfanya yeye aliyechechemea kuwa mabaki, na yeye aliyetupwa mbali kuwa taifa lenye nguvu, na Bwana atawamiliki katika mlima Sayuni tangu sasa na hata milele. 8 Na wewe, Ee mnara wa kundi, kilima cha binti Sayuni, utajiliwa; naam, mamlaka ya kwanza yatakuja, ufalme wa binti Yerusalemu. 9 Sasa mbona unapiga kelele? Je! Hakuna mfalme kwako, mshauri wako amepotea, hata umeshikwa na utungu kama mwanamke wakati wa kuzaa? 10 Uwe na utungu, utaabike ili uzae, Ee binti Sayuni, kama mwanamke mwenye utungu; maana sasa utatoka mjini, nawe utakaa katika mashamba; utafika hata Babeli; huko ndiko utakakookolewa; huko ndiko Bwana atakakokukomboa katika mikono ya adui zako. 11 Na sasa mataifa mengi wamekusanyika juu yako, wasemao, Na atiwe unajisi; macho yetu na yaone shari ya Sayuni. 12 Lakini wao hawayajui mawazo ya Bwana, wala hawafahamu shauri lake; kwa maana amewakusanya kama miganda sakafuni. 13 Haya, simama upure, Ee binti Sayuni; kwa maana nitafanya pembe yako kuwa chuma, na kwato zako kuwa shaba; nawe utaponda-ponda mataifa mengi, na faida yao utaiweka wakfu kwa Bwana, na mali zao kwa Bwana wa dunia yote.

Mika 5

1 Sasa utajikusanya vikosi vikosi, Ee binti wa vikosi; yeye amemhusuru; watampiga mwamuzi wa Israeli shavuni mwake kwa fimbo. 2 Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele. 3 Kwa sababu hiyo atawatoa, hata wakati wa kuzaa kwake aliye na utungu; ndipo hayo mabaki ya nduguze watawarudia wana wa Israeli. 4 Naye atasimama, na kulisha kundi lake kwa nguvu za Bwana, kwa enzi ya jina la Bwana, Mungu wake; nao watakaa; maana sasa atakuwa mkuu hata miisho ya dunia. 5 Na mtu huyu atakuwa amani yetu; wakati Mwashuri atakapoingia katika nchi yetu, na kuyakanyaga majumba yetu, hapo mtaondokesha wachungaji saba juu yake, na wakuu wanane. 6 Nao wataiharibu nchi ya Ashuru kwa upanga, na nchi ya Nimrodi katika malango yake; naye atatuokoa na Mwashuri, atakapoingia katika nchi yetu, na kukanyaga ndani ya mipaka yetu. 7 Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya kabila nyingi mfano wa umande utokao kwa Bwana, mfano wa manyunyu katika manyasi; yasiyomngojea mtu, wala kuwakawilia wanadamu. 8 Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya mataifa, kati ya kabila nyingi, mfano wa simba kati ya wanyama wa msituni, kama mwana-simba kati ya makundi ya kondoo, ambaye, akiwa anapita katikati, hukanyaga-kanyaga na kurarua-rarua, wala hakuna wa kuokoa. 9 Mkono wako na uinuliwe juu ya adui zako, na adui zako wote wakauliwe mbali. 10 Kisha itakuwa katika siku hiyo, asema Bwana, nitawakatilia mbali farasi zako watoke kati yako, nami nitayaharibu magari yako ya vita; 11 nami nitaikatilia mbali miji ya nchi yako, na ngome zako zote nitaziangusha; 12 nami nitakatilia mbali uchawi, usiwe mkononi mwako; wala hutakuwa tena na watu wenye kutabana; 13 nami nitakatilia mbali sanamu zako na nguzo zako, zitoke kati yako; wala hutaiabudu tena kazi ya mikono yako. 14 Nami nitayang'oa maashera yenu, yasiwe kati yako; nami nitaiangamiza miji yako. 15 Nami nitajilipiza kisasi katika hasira na ghadhabu juu ya mataifa wasiosikiliza.

Mika 6

1 Basi sasa, sikieni asemavyo Bwana; Simama, ujitetee mbele ya milima, vilima navyo na visikie sauti yako. 2 Sikieni, enyi milima, mateto ya Bwana, na ninyi, enyi misingi ya dunia iliyo imara; kwa maana Bwana ana mateto na watu wake, naye atahojiana na Israeli. 3 Enyi watu wangu, nimewatenda nini? Nami nimewachosha kwa habari gani? Shuhudieni juu yangu. 4 Kwa maana nalikupandisha kutoka nchi ya Misri, na kukukomboa utoke katika nyumba ya utumwa, nami naliwapeleka Musa, na Haruni, na Miriamu, watangulie mbele yako. 5 Enyi watu wangu, kumbukeni sasa alivyouliza Balaki, mfalme wa Moabu, na alivyojibu Balaamu, mwana wa Beori; kumbukeni toka Shitimu hata Gilgali, mpate kuyajua matendo ya haki ya Bwana. 6 Nimkaribie Bwana na kitu gani, na kuinama mbele za Mungu aliye juu? Je! Nimkaribie na sadaka za kuteketezwa, na ndama za umri wa mwaka mmoja? 7 Je! Bwana atapendezwa na elfu za kondoo waume, au na elfu kumi za mito ya mafuta? Je! Nimtoe mzaliwa wangu wa kwanza kwa kosa langu, mzao wa mwili wangu kwa dhambi ya roho yangu? 8 Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako! 9 Sauti ya Bwana inaulilia mji, na mtu mwenye akili ataliona jina lako; isikieni hiyo fimbo na yeye aliyeiagiza. 10 Je! Hata sasa hazina za uovu zingalimo nyumbani mwa wabaya, na kipimo kilichopunguka, ambacho ni chukizo? 11 Je! Naweza kuwa safi nami nina mizani ya udhalimu, na mfuko wa mawe ya kupimia ya udanganyifu? 12 Kwa maana matajiri wake wamejaa jeuri, na wenyeji wake wamesema uongo, na ulimi wao una udanganyifu kichwani mwao. 13 Basi, kwa ajili ya hayo, mimi nami nimekupiga kwa pigo liumizalo sana; nimekufanya kuwa ukiwa, kwa sababu ya dhambi zako. 14 Utakula, lakini hutashiba; na fedheha yako itakuwa kati yako; nawe utahama, lakini hutachukua kitu salama; na hicho utakachochukua nitakitoa kwa upanga. 15 Utapanda, lakini hutavuna; utazikanyaga zeituni, lakini hutajipaka mafuta; na hizo zabibu, lakini hutakunywa divai. 16 Kwa maana amri za Omri ndizo zishikwazo, na matendo yote ya nyumba ya Ahabu, nanyi mnakwenda katika mashauri yao; ili nikufanye kuwa ukiwa, na wenyeji waliomo humo kuwa zomeo; nanyi mtayachukua matukano waliyotukanwa watu wangu.

Mika 7

1 Ole wangu! Maana mimi ni kama hapo walipokwisha kuyachuma matunda ya wakati wa hari, kama zabibu zichumwazo baada ya mavuno; hapana shada la kuliwa; roho yangu inatamani tini iivayo kwanza. 2 Mtu amchaye Mungu ametoweka, asionekane katika nchi, wala hapana mtu mwenye adili katika wanadamu; wote huotea ili kumwaga damu; kila mtu humwinda ndugu yake kwa wavu. 3 Mikono yao inayashika mabaya wayatende kwa bidii; mtu mkuu aomba rushwa, kadhi yu tayari kuipokea; mtu mkubwa hunena madhara yaliyomo rohoni mwake; hivyo ndivyo wayafumavyo hayo pamoja. 4 Mtu aliye mwema miongoni mwao ni kama mbigili; mtu aliye mwenye adili miongoni mwao ni mbaya kuliko boma la michongoma; hiyo siku ya walinzi wako, yaani, siku ya kujiliwa kwako, imefika; sasa kutatokea kufadhaika kwao. 5 Msimwamini rafiki, msimwekee kiongozi tumaini; ilinde milango ya midomo ya kinywa chako ili mkeo alalaye kifuani mwako asijue habari. 6 Kwa maana mwana humwaibisha babaye, na binti huondoka ashindane na mamaye; na mwanamke aliyeolewa hushindana na mavyaaye; adui za mtu ni watu wa nyumbani mwake mwenyewe. 7 Lakini mimi, nitamtazamia Bwana; nitamngojea Mungu wa wokovu wangu; Mungu wangu atanisikia. 8 Usifurahi juu yangu, Ee adui yangu; niangukapo, nitasimama tena; nikaapo gizani, Bwana atakuwa nuru kwangu. 9 Nitaivumilia ghadhabu ya Bwana, kwa kuwa nimemwasi; hata atakaponitetea teto langu, na kunifanyia hukumu; atanileta nje kwenye nuru, nami nitaiona haki yake. 10 Ndipo adui yangu ataliona jambo hilo, na aibu itamfunika, yeye aliyeniambia, Yuko wapi Bwana, Mungu wako? Macho yangu yatamtazama; sasa atakanyagwa kama matope ya njia kuu. 11 Ni siku ya kujengwa kuta zako! Siku hiyo mpaka utasongezwa mbali. 12 Siku hiyo watakujia kutoka Ashuru na miji ya Misri, na kutoka Misri mpaka huo Mto, na kutoka bahari hii mpaka bahari hii, na kutoka mlima huu mpaka mlima huu. 13 Hata hivyo nchi itakuwa ukiwa kwa sababu ya hao wakaao ndani yake, kwa sababu ya matunda ya matendo yao. 14 Walishe watu wako kwa fimbo yako, kundi la urithi wako, wakaao peke yao, mwituni katikati ya Karmeli; na walishe katika Bashani na Gileadi, kama siku za kale. 15 Kama katika siku zile za kutoka kwako katika nchi ya Misri nitamwonyesha mambo ya ajabu. 16 Mataifa wataona, na kuzitahayarikia nguvu zao zote; wataweka mikono yao juu ya vinywa vyao, masikio yao yatakuwa na uziwi. 17 Watayaramba mavumbi kama nyoka, kama vitu vitambaavyo juu ya nchi watatoka katika mahali walimojificha, wakitetemeka; watakuja kwa Bwana, Mungu wetu, kwa hofu, nao wataogopa kwa sababu yako. 18 Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema. 19 Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari. 20 Wewe utamtimilizia Yakobo kweli yako, na Ibrahimu rehema zako, ulizowaapia baba zetu tangu siku za kale.

Nahumu 1

1 Ufunuo juu ya Ninawi. Kitabu cha maono aliyoyaona Nahumuu, Mwelkoshi. 2 Bwana ni Mungu mwenye wivu, naye hujilipiza kisasi; Bwana hujilipiza kisasi, naye ni mwingi wa hasira; Bwana hujilipiza kisasi juu ya adui zake, huwawekea adui zake akiba ya hasira. 3 Bwana si mwepesi wa hasira, ana uweza mwingi, wala hatamhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; Bwana ana njia yake katika kisulisuli na tufani, na mawingu ni mavumbi ya miguu yake. 4 Yeye huikemea bahari na kuikausha, pia huikausha mito yote; Bashani hulegea, na Karmeli; hulegea nalo ua la Lebanoni. 5 Milima hutetema mbele zake, navyo vilima huyeyuka; nayo dunia huinuliwa mbele za uso wake, naam, dunia na wote wakaao ndani yake. 6 Ni nani awezaye kusimama mbele za ghadhabu yake, naye ni nani awezaye kukaa katika ukali wa hasira yake? Hasira yake kali humwagwa kama moto, nayo majabali yapasuliwa na yeye. 7 Bwana ni mwema, ni ngome siku ya taabu; naye huwajua hao wamkimbiliao. 8 Lakini kwa gharika ifurikayo atapakomesha kabisa mahali pake, na kuwafuatia adui zake hata gizani. 9 Mnawaza nini juu ya Bwana? Yeye atakomesha kabisa; mateso hayatainuka mara ya pili. 10 Kwa maana wangawa kama miiba iliyotatana, na kunyweshwa kana kwamba ni katika kunywa kwao, wataliwa kabisa kama mabua makavu. 11 Ametoka mmoja kwako, aniaye mabaya juu ya Bwana, atoaye mashauri yasiyofaa kitu. 12 Bwana asema hivi, Ijapokuwa wana nguvu zilizo timilifu, ijapokuwa ni wengi, hata hivyo watakatwa, naye atapita na kwenda zake. Ingawa nimekutesa, sitakutesa tena. 13 Na sasa nitakuvunjia nira yake, nami nitakupasulia mafungo yako. 14 Tena Bwana ametoa amri katika habari zako, ya kwamba asipandwe tena mtu awaye yote mwenye jina lako; toka nyumba ya miungu yako nitakatilia mbali sanamu ya kuchora, na sanamu ya kuyeyusha; nitakufanyia kaburi lako; kwa maana u mbovu. 15 Tazama, juu ya milima iko miguu yake aletaye habari njema, atangazaye amani. Zishike sikukuu zako, Ee Yuda, uziondoe nadhiri zako; kwa maana yule asiyefaa kitu hatapita kati yako tena kamwe; amekwisha kukatiliwa mbali.

Nahumu 2

1 Yeye asetaye vipande vipande amepanda juu mbele ya uso wako; zishike silaha, ilinde njia, vitie nguvu viuno vyako, uongeze uwezo wako sana. 2 Kwa maana Bwana anairudisha fahari ya Yakobo, kama fahari ya Israeli; maana watekao nyara wamewateka, na kuyaharibu matawi ya mizabibu yao. 3 Ngao ya mashujaa wake imefanywa kuwa nyekundu, watu walio hodari wa vita wamevaa nguo nyekundu sana; magari ya vita yametameta kwa chuma cha pua siku ya kujitengeza kwake, na mikuki inatikiswa kwa namna ya kutisha. 4 Magari ya vita yanafanya mshindo njiani, Yanasongana-songana katika njia kuu; Kuonekana kwake ni kama mienge, Yanakwenda upesi kama umeme. 5 Awakumbuka watu wake wenye heshima; Wanajikwaa katika mwendo wao; Wanafanya haraka waende ukutani; Nacho kitu cha kuwafunika kimewekwa tayari. 6 Malango ya mito yamefunguka, na jumba la mfalme limeyeyushwa. 7 Husabu naye amefunuliwa, anachukuliwa, na wajakazi wake wanalia kama kwa sauti ya hua, wakipiga-piga vifua vyao. 8 Lakini Ninawi tokea zamani amekuwa kama ziwa la maji; ila hata sasa wanakimbia; Simameni! Simameni! Lakini hapana hata mmoja atazamaye nyuma. 9 Chukueni nyara za fedha; Chukueni nyara za dhahabu; Kwa maana ni akiba isiyoisha, Fahari ya vyombo vipendezavyo. 10 Amekuwa utupu, na ukiwa, na uharibifu; hata moyo unayeyuka, na magoti yanagongana-gongana; viunoni mwote mna utungu, na nyuso za wote zimekuwa nyeupe kwa hofu. 11 Kao la simba li wapi? Na mahali walishapo wana-simba pa wapi, mahali walipotembea simba mume na simba mke na mwana-simba, wala hapana aliyewatia hofu? 12 Simba alirarua vipande vipande chakula cha kuwatosha watoto wake, aliwasongea wake zake nyama, aliyajaza mapango yake mateka, na makao yake aliyajaza mawindo. 13 Tazama, mimi ni juu yako, asema Bwana wa majeshi, nami nitayateketeza magari yako ya vita katika moshi, na upanga utawala wana-simba wako; nami nitayakatilia mbali mawindo yako katika nchi, na sauti za wajumbe wako hazitasikiwa tena kamwe.

Nahumu 3

1 Ole wake mji wa damu! Umejaa mambo ya uongo na unyang'anyi; mateka hayaondoki. 2 Kelele za mjeledi, kelele za magurudumu yafanyayo kishindo; na farasi wenye kupara-para, na magari ya vita yenye kuruka-ruka; 3 mpanda farasi akipanda, na upanga ukimeta-meta, na mkuki ukimemetuka; na wingi wa waliouawa, na chungu kubwa ya mizoga; mizoga haina mwisho; wanajikwaa juu ya mizoga yao. 4 Kwa sababu ya wingi wa ukahaba wa yule kahaba mzuri, yule bibi wa mambo ya uchawi, auzaye mataifa kwa ukahaba wake, na jamaa za watu kwa uchawi wake. 5 Tazama, mimi ni juu yako, asema Bwana wa majeshi; nami nitafunua marinda yako mbele ya uso wako; nami nitawaonyesha mataifa uchi wako, na falme aibu yako. 6 Nami nitatupa uchafu uchukizao juu yako, kukufanya uwe mchafu, nami nitakufanya kuwa kitu cha kutazamwa kwa dharau. 7 Hata itakuwa, wote wakutazamao watakukimbia, wakisema, Ninawi umeharibika; ni nani atakayeuhurumia? Nikutafutie wapi wafariji? 8 Je! Wewe u mwema kuliko No-amoni, uliowekwa kati ya mito, uliozungukwa na maji; ambao boma lake lilikuwa bahari, na bahari ilikuwa ukuta wake. 9 Kushi na Misri walikuwa nguvu zake, nazo zilikuwa hazina mpaka; Putu na Walibia walikuwa wasaidizi wake. 10 Hata hivyo alichukuliwa mbali, alikwenda utumwani; watoto wake wachanga walisetwa kwenye maachano ya njia kuu zote; watu wake wenye heshima wakapigiwa kura, na wakuu wake wote wakafungwa kwa minyororo. 11 Tena utalewa, utafichwa; tena utatafuta ngome kwa sababu ya adui. 12 Ngome zako zote zitakuwa kama mitini yenye tini zilizoiva kwanza; ikitikisika zaanguka katika kinywa chake alaye. 13 Tazama, watu wako walio ndani yako ni wanawake; malango ya nchi yako yamekuwa wazi kabisa mbele ya adui zako; moto umeteketeza mapingo yako. 14 Teka maji yawe tayari kwa kuzingirwa kwako; Zitie nguvu ngome zako; Ingia katika udongo, yakanyage matope, Itie nguvu tanuru ya kuokea matofali. 15 Huko moto utakuteketeza; Upanga utakukatilia mbali; Utakumeza kama tunutu alavyo; Jifanye kuwa wengi kama tunutu! Jifanye kuwa wengi kama nzige! 16 Umeongeza wafanya biashara wako kuwa wengi kuliko nyota za mbinguni; tunutu huharibu; kisha huruka juu na kwenda zake. 17 Watu wako waliotiwa taji ni kama nzige, na majemadari wako ni kama makundi ya mapanzi, watuao katika vitalu siku ya baridi, lakini jua lipandapo huruka juu na kwenda zao, na mahali pao walipo hapajulikani. 18 Wachungaji wako wanalala usingizi, Ee mfalme wa Ashuru; watu wako wenye heshima wamepumzika; watu wako wametawanyika juu ya milima, wala hapana mtu wa kuwakusanya. 19 Jeraha yako haipunguziki; jeraha yako ni nzito sana; wote wasikiao habari zako wapiga makofi juu yako; kwa maana ni nani ambaye uovu wako haukupita juu yake daima?

Habakuki 1

1 Ufunuo aliouona nabii Habakuki. 2 Ee Bwana, nilie hata lini, wewe usitake kusikia? Nakulilia kwa sababu ya udhalimu, ila hutaki kuokoa. 3 Mbona wanionyesha uovu, na kunitazamisha ukaidi? Maana uharibifu na udhalimu u mbele yangu; kuna ugomvi, na mashindano yatokea. 4 Kwa sababu hiyo sheria imelegea, wala hukumu haipatikani; kwa maana watu wabaya huwazunguka wenye haki; kwa sababu hiyo hukumu ikipatikana imepotoka. 5 Angalieni, enyi mlio kati ya mataifa, katazameni, kastaajabuni sana; kwa maana mimi natenda tendo siku zenu, ambalo hamtaliamini hata mkiambiwa. 6 Kwa maana, angalieni, nawaondokesha Wakaldayo, taifa lile kali, lenye haraka kupita kiasi; wapitao katikati ya dunia, ili wayamiliki makao yasiyo yao. 7 Hao ni watu wa kutisha sana, wa kuogofya sana; hukumu yao na ukuu wao hutoka katika nafsi zao wenyewe. 8 Farasi zao ni wepesi kuliko chui, ni wakali kuliko mbwa-mwitu wa jioni; na wapanda farasi wao hujitapa naam, wapanda farasi wao watoka mbali sana; huruka kama tai afanyaye haraka ale. 9 Waja wote ili kufanya udhalimu; nyuso zao zimeelekezwa kwa bidii yao kama upepo wa mashariki, nao hukusanya mateka kama mchanga. 10 Naam, huwadhihaki wafalme, na wakuu ni kitu cha kudharauliwa kwake; huidharau kila ngome; kwa maana hufanya chungu ya mavumbi, na kuitwaa. 11 Kisha atapita kwa kasi, kama upepo, atapita na kuwa ana hatia; yeye ambaye nguvu zake ni mungu wake. 12 Ee Bwana, Mungu wangu, mtakatifu wangu, wewe si wa milele? Hatutakufa. Ee Bwana, umemwandikia hukumu, nawe, Ee Jabali, umemweka imara ili aadhibishwe. 13 Wewe uliye na macho safi hata usiweze kuangalia uovu, wewe usiyeweza kutazama ukaidi, mbona unawaangalia watendao kwa hila; na kunyamaza kimya, hapo mtu mwovu ammezapo mtu aliye mwenye haki kuliko yeye; 14 na kufanya wanadamu kuwa kama samaki wa baharini, kama vitu vitambaavyo, ambavyo havina mtawala? 15 Yeye huwatoa wote kwa ndoana yake, huwakamata katika wavu wake, na kuwakusanya katika juya lake; ndiyo sababu afurahi na kupendezwa. 16 Kwa sababu hiyo huutolea wavu wake sadaka, na kulifukizia uvumba juya lake; kwa sababu kwa vitu vile fungu lake limenona, na chakula chake kimekuwa tele. 17 Je! Atawatoa walio katika wavu wake, asiache kuwaua watu wa mataifa daima?

Habakuki 2

1 Mimi nitasimama katika zamu yangu, nitajiweka juu ya mnara, nitaangalia ili nione atakaloniambia, na jinsi nitakavyojibu katika habari ya kulalamika kwangu. 2 Bwana akanijibu, akasema, Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji. 3 Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia. 4 Tazama, roho yake hujivuna, haina unyofu ndani yake; lakini mwenye haki ataishi kwa imani yake. 5 Naam, pamoja na hayo, divai ni mchumi mdanganyifu, mtu wa kiburi asiyekaa nyumbani mwake; huongeza tamaa yake kama kuzimu, naye huwa kama mauti, hawezi kushibishwa; bali hujikusanyia mataifa yote; hujiwekea kabila zote chungu chungu. 6 Je! Hawa wote hawatapiga mfano juu yake, na mithali ya kusimanga juu yake, wakisema, Ole wake yeye aongezaye kisicho mali yake! Hata lini? Na ole wake yeye ajitwikaye mzigo wa rehani! 7 Je! Hawatainuka ghafula wao watakaokuuma, hawataamka wao watakaokusumbua, nawe utakuwa mateka kwao? 8 Kwa sababu umeteka nyara mataifa mengi, mabaki yote ya kabila watakuteka wewe; kwa sababu ya damu ya watu, na kwa sababu ya udhalimu iliotendwa nchi hii, na mji huu, na watu wote wanaokaa ndani yake. 9 Ole wake yeye aipatiaye nyumba yake mapato mabaya, ili apate kukiweka kioto chake juu, apate kujiepusha na mkono wa uovu! 10 Wewe umeifanyia nyumba yako kusudi la aibu, kwa kukatilia mbali watu wengi, nawe umetenda dhambi juu ya roho yako. 11 Kwa maana jiwe litapiga kelele katika ukuta, nayo boriti katika miti italijibu. 12 Ole wake yeye ajengaye mji kwa damu, awekaye imara mji mkubwa kwa uovu! 13 Angalieni; je! Jambo hili halikutoka kwa Bwana wa majeshi, kwamba watu wajishughulikie moto, na mataifa wajisumbue kwa ajili ya ubatili? 14 Kwa maana dunia itajazwa maarifa ya utukufu wa Bwana, kama maji yaifunikavyo bahari. 15 Ole wake yeye ampaye jirani yake kileo, wewe utiaye sumu yako, na kumlevya pia, ili kuutazama uchi wao! 16 Umejaa aibu badala ya utukufu; unywe nawe, uwe kama mtu asiyetahiriwa; kikombe cha mkono wa kuume wa Bwana kitageuzwa ukipokee, na aibu kuu itakuwa juu ya utukufu wako. 17 Kwa maana udhalimu uliotendwa juu ya Lebanoni utakufunikiza, na kuangamizwa kwao wanyama kutakutia hofu; kwa sababu ya damu ya watu, na kwa sababu ya udhalimu iliotendwa nchi hii, na mji huu, na watu wote wanaokaa ndani yake. 18 Sanamu ya kuchora yafaa nini, hata yeye aliyeifanya ameichora? Sanamu ya kuyeyuka, nayo ni mwalimu wa uongo, yafaa nini, hata yeye aliyeifanya aiwekee tumaini lake, na kufanya sanamu zisizoweza kusema? 19 Ole wake yeye auambiaye mti, Amka; aliambiaye jiwe lisiloweza kusema, Ondoka! Je! Kitu hicho kitafundisha? Tazama, kimefunikwa kwa dhahabu na fedha, wala hamna pumzi ndani yake kabisa. 20 Lakini Bwana yumo ndani ya hekalu lake takatifu; dunia yote na inyamaze kimya mbele zake.

Habakuki 3

1 Sala ya nabii Habakuki. 2 Ee Bwana, nimesikia habari zako, nami naogopa; Ee Bwana, fufua kazi yako katikati ya miaka; Katikati ya miaka tangaza habari yake; Katika ghadhabu kumbuka rehema. 3 Mungu alikuja kutoka Temani, Yeye aliye mtakatifu kutoka mlima Parani. Utukufu wake ukazifunika mbingu, Nayo dunia ikajaa sifa yake. 4 Mwangaza wake ulikuwa kama nuru; Alikuwa na mishale ya nuru ubavuni pake; Ndipo ulipofichwa uweza wake. 5 Mbele zake ilikwenda tauni, Na makaa ya moto yakatoka miguuni pake. 6 Akasimama, akaitetemesha dunia; Akatazama, akawasitusha mataifa; Na milima ya zamani ikatawanyika; Vilima vya kale vikainama; Miendo yake ilikuwa kama siku za kale. 7 Naliziona hema za Kushani katika taabu; Mapazia ya nchi ya Midiani yakatetemeka. 8 Je! Bwana aliikasirikia mito? Je! Hasira yako ilikuwa juu ya mito, Au ghadhabu yako juu ya bahari, Hata ukapanda farasi zako, Katika magari yako ya wokovu? 9 Uta wako ukafanywa wazi kabisa; Viapo walivyopewa kabila vilikuwa neno thabiti; Ukaipasua nchi kwa mito. 10 Milima ilikuona, ikaogopa; Gharika ya maji ikapita; Vilindi vikatoa sauti yake, Vikainua juu mikono yake. 11 Jua na mwezi vikasimama makaoni mwao; Mbele ya nuru ya mishale yako ilipotapakaa, Mbele ya mwangaza wa mkuki wako umeremetao. 12 Ulikwenda katikati ya nchi kwa ghadhabu; Ukawapura mataifa kwa hasira. 13 Ukatokea kwa ajili ya wokovu wa watu wako, Kwa ajili ya wokovu wa masihi wako; Ukakiponda kichwa cha nyumba ya waovu, Ukiuweka wazi msingi hata mwambani. 14 Ukakichoma kichwa cha mashujaa wake kwa fimbo zao wenyewe; Wakaja kama kisulisuli ili kunitawanya; Kama wakifurahi kuwameza maskini kwa siri. 15 Ukaikanyaga bahari kwa farasi zako, Chungu ya maji yenye nguvu. 16 Nikasikia, na tumbo langu likatetemeka, Midomo yangu ikatikisika kwa sauti ile; Ubovu ukaingia mifupani mwangu, Nikatetemeka katika mahali pangu; Ili nipate kuingoja ile siku ya dhiki, Kundi lao washambuliao wakweapo juu ya watu. 17 Maana mtini hautachanua maua, Wala mizabibuni hamtakuwa na matunda; Taabu ya mzeituni itakuwa bure, Na mashamba hayatatoa chakula; Zizini hamtakuwa na kundi, Wala vibandani hamtakuwa na kundi la ng'ombe; 18 Walakini nitamfurahia Bwana Nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.

Sefania 1

1 Neno la Bwana lililomjia Sefania, mwana wa Kushi, mwana wa Gedalia, mwana wa Amaria, mwana wa Hezekia; katika siku za Yosia, mwana wa Amoni, mfalme wa Yuda. 2 Nitavikomesha kabisa vitu vyote, visionekane juu ya uso wa nchi, asema Bwana. 3 Nitamkomesha mwanadamu na mnyama; nitakomesha ndege wa angani, na samaki wa baharini, na hayo makwazo pamoja na wabaya; nami nitamkatilia mbali mwanadamu, asionekane juu ya uso wa nchi, asema Bwana. 4 Nami nitaunyosha mkono wangu juu ya Yuda, na juu ya watu wote wakaao Yerusalemu; nami nitayakatilia mbali mabaki ya Baali, yasionekane mahali hapa, na hilo jina la Wakemari pamoja na makuhani; 5 na wale walisujudiao jeshi la mbinguni juu ya dari za nyumba; na hao waabuduo, waapao kwa Bwana na kuapa pia kwa Malkamu; 6 na hao waliorudi nyuma, na kuacha kumfuata Bwana; na hao wasiomtafuta Bwana, wala kumwulizia. 7 Nyamaza kimya mbele za Bwana MUNGU; Kwa maana siku ya Bwana i karibu; Kwa kuwa Bwana ameweka tayari dhabihu, Amewatakasa wageni wake. 8 Na itakuwa, katika siku ile ya dhabihu ya Bwana, nitawaadhibu wakuu, na wana wa mfalme, na watu wote waliovaa mavazi ya kigeni. 9 Na katika siku ile nitawaadhibu hao wote warukao juu ya kizingiti, waijazao nyumba ya bwana wao udhalimu na udanganyifu. 10 Na katika siku ile, asema Bwana kutakuwako sauti ya kilio kutoka lango la samaki, na mlio mkuu katika mtaa wa pili, na mshindo mkuu kutoka milimani. 11 Haya! Lieni, ninyi mkaao katika Makteshi, maana wafanya biashara wote wameangamia; hao wote waliokuwa na mizigo ya fedha wamekatiliwa mbali. 12 Kisha itakuwa wakati ule, nitauchunguza Yerusalemu kwa taa; nami nitawaadhibu watu walioganda juu ya sira zao; wasemao katika mioyo yao, Bwana hatatenda mema, wala hatatenda mabaya. 13 Na huko utajiri wao utakuwa mateka, na nyumba zao zitakuwa ukiwa; naam, watajenga nyumba, lakini hawatakaa ndani yake; nao watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake. 14 Hiyo siku ya Bwana iliyo kuu i karibu; I karibu, nayo inafanya haraka sana; Naam, sauti ya siku ya Bwana; Shujaa hulia kwa uchungu mwingi huko! 15 Siku ile ni siku ya ghadhabu, Siku ya fadhaa na dhiki, Siku ya uharibifu na ukiwa, Siku ya giza na utusitusi, Siku ya mawingu na giza kuu, 16 Siku ya tarumbeta na ya kamsa, Juu ya miji yenye maboma, Juu ya buruji zilizo ndefu sana. 17 Nami nitawaletea wanadamu dhiki, hata watakwenda kama vipofu, kwa sababu wamemtenda Bwana dhambi; na damu yao itamwagwa kama mavumbi, na nyama yao kama mavi. 18 Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya Bwana; bali nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi hii, naam, ukomo wa kutisha.

Sefania 2

1 Jikusanyeni, naam, jikusanyeni, Ee taifa lisilo na haya; 2 kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya Bwana, kabla haijawajilia siku ya hasira ya Bwana. 3 Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya Bwana. 4 Kwa kuwa Gaza utaachwa, na Ashkeloni utakuwa ukiwa; wataufukuzia mbali Ashdodi wakati wa adhuhuri, na Ekroni utang'olewa. 5 Ole wao wakaao karibu na pwani ya bahari, taifa la Wakerethi! Neno la Bwana li juu yenu, Ee Kanaani, nchi ya Wafilisti; mimi nitakuangamiza, asibaki mtu akaaye kwako. 6 Na hiyo nchi ya pwani itakuwa malisho, yenye vibanda vya wachungaji, na mazizi ya makundi ya kondoo. 7 Na hiyo nchi ya pwani itakuwa nchi ya watu wa nyumba ya Yuda waliosalia; watalisha makundi yao huko; watalala katika nyumba za Ashkeloni wakati wa jioni; kwa maana Bwana, Mungu wao, atawajilia na kuwarudisha wafungwa wao. 8 Mimi nimeyasikia matukano ya Moabu, na dhihaka za wana wa Amoni, ambazo kwa hizo wamewatukana watu wangu, na kujitukuza juu ya mpaka wao. 9 Basi kama niishivyo, asema Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, Hakika Moabu atakuwa kama Sodoma, na wana wa Amoni kama Gomora, yaani, milki ya upupu, na mashimo ya chumvi, ukiwa wa daima; watu wangu waliosalia watawateka nyara, na watu wa taifa langu waliobaki watawarithi. 10 Mambo hayo yatawapata kwa sababu ya kiburi chao, kwa kuwa wamewatukana watu wa Bwana wa majeshi, na kujitukuza juu yao. 11 Bwana atakuwa mwenye kuwatisha sana; kwa maana atawafisha kwa njaa miungu yote ya dunia; na watu watamsujudia yeye, kila mtu toka mahali pake; naam, nchi zote za mataifa. 12 Na ninyi Wakushi pia, mtauawa kwa upanga wangu. 13 Naye atanyosha mkono wake juu ya upande wa kaskazini, na kuiangamiza Ashuru; naye ataufanya Ninawi kuwa ukiwa, kuwa mahali pakavu kama jangwa. 14 Na makundi ya wanyama watalala kati yake, wanyama wote wa mataifa; mwari-nyuni na nungu watakaa juu ya vichwa vya nguzo zake; sauti yao itasikiwa madirishani; vizingitini mwake mtakuwa ukiwa; kwa maana ameifunua kazi ya mierezi. 15 Huu ndio mji ule wa furaha, Uliokaa pasipo kufikiri, Uliosema moyoni mwake, Mimi niko, Wala hapana mwingine ila mimi. Jinsi ulivyokuwa ukiwa, Mahali pa kulala pa wanyama wa bara! Kila mtu apitaye atazomea, Na kutikisa mkono wake.

Sefania 3

1 Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa udhalimu! 2 Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa; hakumwamini Bwana; hakumkaribia Mungu wake. 3 Wakuu wake walio ndani yake ni simba wangurumao; makadhi wake ni mbwa-mwitu wa jioni; hawasazi kitu cho chote hata siku ya pili. 4 Manabii wake ni watu hafifu, wadanganyifu; makuhani wake wamepatia unajisi patakatifu, wameifanyia sheria udhalimu. 5 Bwana kati yake ni mwenye haki; hatatenda uovu; kila asubuhi hudhihirisha hukumu yake, wala hakomi; bali mtu asiye haki hajui kuona haya. 6 Nimekatilia mbali mataifa, buruji zao zina ukiwa; nimeziharibu njia kuu zao, hata hapana mmoja apitaye; miji yao imeangamizwa; hamna mtu hata mmoja, wala hapana akaaye huko. 7 Nalisema, Hakika utaniogopa, utakubali kurudiwa; ili yasikatiliwe mbali makao yake, sawasawa ya yote niliyoagiza katika habari zake; lakini waliondoka mapema na kuyaharibu matendo yao yote. 8 Basi ningojeni, asema Bwana, hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu. 9 Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la Bwana, wamtumikie kwa nia moja. 10 Maana toka nchi iliyo mbali na mito ya Kushi, waniombao dua, yaani, binti za watu wangu waliotawanyika, wataleta matoleo yangu. 11 Siku ile hutatahayarikia matendo yako yote uliyoniasi; maana hapo nitawaondoa watu wako wanaotakabari na kujivuna, wasiwe kati yako, wala hutatakabari tena katika mlima wangu mtakatifu. 12 Lakini nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la Bwana. 13 Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya. 14 Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; Furahi na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu. 15 Bwana ameziondoa hukumu zako, Amemtupa nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa uovu tena. 16 Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, Usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee. 17 Bwana, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; Atakushangilia kwa furaha kuu, Atakutuliza katika upendo wake, Atakufurahia kwa kuimba. 18 Nitawakusanya wanaousikitikia mkutano wa ibada, hao waliokuwa wa kwako; ambao mzigo uliokuwa juu yake ulikuwa fedheha kwao. 19 Tazama, wakati huo nitawapatiliza watu wote wanaokutesa; nami nitamponya yeye achechemeaye, nami nitamkusanya yeye aliyefukuzwa; nami nitawafanya kuwa sifa na jina, hao ambao fedheha yao ilikuwa katika dunia yote. 20 Wakati huo nitawaingizeni, na wakati huo nitawakusanya; kwa maana nitawafanya ninyi kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia, nitakapowarudisha wafungwa wenu mbele ya macho yenu, asema Bwana.

Hagai 1

1 Katika mwaka wa pili wa Dario mfalme, mwezi wa sita, siku ya kwanza ya mwezi, neno la Bwana lilimjia Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, liwali wa Yuda, na Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, kwa kinywa chake Hagai nabii, kusema, 2 Bwana wa majeshi asema hivi, ya kwamba, Watu hawa husema, Huu sio wakati utupasao kuja, huu sio wakati wa kujenga nyumba ya Bwana. 3 Ndipo neno la Bwana lilikuja kwa kinywa cha nabii Hagai, kusema, 4 Je! Huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika? 5 Basi sasa, Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu. 6 Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka. 7 Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu. 8 Pandeni milimani, mkalete miti, mkaijenge nyumba; nami nitaifurahia, nami nitatukuzwa, asema Bwana. 9 Mlitazamia vingi, kumbe vikatokea vichache; tena mlipovileta nyumbani nikavipeperusha. Ni kwa sababu gani? Asema Bwana wa majeshi. Ni kwa sababu ya nyumba yangu inayokaa hali ya kuharibika, wakati ambapo ninyi mnakimbilia kila mtu nyumbani kwake. 10 Basi, kwa ajili yenu mbingu zimezuiliwa zisitoe umande, nayo nchi imezuiliwa isitoe matunda yake. 11 Nami nikaita wakati wa joto uje juu ya nchi, na juu ya milima, na juu ya nafaka, na juu ya divai mpya, na juu ya mafuta, na juu ya kila kitu itoacho nchi, na juu ya wanadamu, na juu ya wanyama, na juu ya kazi zote za mikono. 12 Ndipo Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, pamoja na hayo mabaki yote ya watu, wakaitii sauti ya Bwana, Mungu wao, na maneno ya Hagai nabii, kama Bwana, Mungu wao, alivyomtuma; nao watu wakaogopa mbele za Bwana. 13 Ndipo Hagai mjumbe wa Bwana, katika ujumbe wa Bwana, akawaambia watu, akisema, Mimi nipo pamoja nanyi, asema Bwana. 14 Bwana akaiamsha roho ya Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, liwali wa Yuda, na roho ya Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, na roho zao mabaki ya watu; wakaenda, wakafanya kazi katika nyumba ya Bwana wa majeshi, Mungu wao; 15 katika siku ya ishirini na nne ya mwezi, katika mwezi wa sita, katika mwaka wa pili wa Dario mfalme.

Hagai 2

1 Katika mwezi wa saba, siku ya ishirini na moja ya mwezi, neno la Bwana lilikuja kwa kinywa cha Hagai nabii, kusema, 2 Sema sasa na Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, liwali wa Yuda, na Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, na hayo mabaki ya watu, ukisema, 3 Miongoni mwenu amebaki nani aliyeiona nyumba hii katika utukufu wake wa kwanza? Nanyi mnaionaje sasa? Je! Mbele ya macho yenu, siyo kama si kitu? 4 Lakini sasa uwe hodari, Ee Zerubabeli, asema Bwana; nawe uwe hodari, Ee Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, nanyi iweni hodari, enyi watu wote wa nchi hii, asema Bwana; mkafanye kazi, kwa kuwa mimi ni pamoja nanyi, asema Bwana wa majeshi; 5 kama neno lile nililoagana nanyi mlipotoka katika nchi ya Misri; na roho yangu inakaa kati yenu; msiogope. 6 Kwa maana Bwana wa majeshi asema hivi, Mara moja tena, ni kitambo kidogo tu, nami nitazitikisa hizo mbingu, na hii nchi, na bahari, na nchi kavu; 7 nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema Bwana wa majeshi. 8 Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa majeshi. 9 Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema Bwana wa majeshi; na katika mahali hapa nitawapa amani, asema Bwana wa majeshi. 10 Siku ya ishirini na nne, ya mwezi wa kenda, katika mwaka wa pili wa Dario, neno la Bwana lilikuja kwa kinywa cha Hagai nabii, kusema, 11 Bwana wa majeshi asema hivi, Waulizeni sasa makuhani katika habari ya sheria, mkisema, 12 Mtu akichukua nyama takatifu katika upindo wa nguo yake, naye akagusa kwa upindo wake mkate, au ugali, au divai, au mafuta, au chakula cho chote, je! Kitu hicho kitakuwa kitakatifu? Makuhani wakajibu, wakasema, La. 13 Ndipo Hagai akasema, Kama mtu aliyetiwa unajisi kwa kugusa maiti, akigusa kimojawapo cha vitu hivi, je! Kitakuwa najisi? Makuhani wakajibu, wakasema, Kitakuwa najisi. 14 Ndipo Hagai akajibu, akasema, Hivyo ndivyo walivyo watu hawa, na hivyo ndivyo lilivyo taifa hili mbele zangu, asema Bwana; na hivyo ndivyo ilivyo kila kazi ya mikono yao; na kitu hicho wakitoacho sadaka huko ni najisi. 15 Na sasa nawaomba, tafakarini; tangu siku hii na siku zilizopita; kabla halijatiwa bado jiwe juu ya jiwe katika nyumba ya Bwana; 16 katika wakati huo wote, mtu alipofikia chungu ya vipimo ishirini, palikuwa na vipimo kumi tu; na mtu alipofikia shinikizo apate kuteka divai ya vyombo hamsini, palikuwa na divai ya vyombo ishirini tu. 17 Naliwapiga kwa ukavu, na ukungu, na mvua ya mawe, katika kazi zote za mikono yenu; lakini hamkunielekea mimi, asema Bwana. 18 Tafakarini, nawaomba; tangu siku hii ya leo na siku zijazo; tangu siku ya ishirini na nne ya mwezi wa kenda, naam, tangu siku hiyo ulipowekwa msingi wa hekalu la Bwana tafakarini haya. 19 Je! Mbegu ingali ghalani? Naam, huo mzabibu, wala mtini, wala mkomamanga, wala mzeituni, haikuzaa kitu; tangu siku hii ya leo nitawabariki. 20 Kisha neno la Bwana likamjia Hagai mara ya pili, siku ya ishirini na nne ya mwezi, kusema, 21 Sema na Zerubabeli, liwali wa Yuda, ukisema, Nitazitikisa mbingu na dunia; 22 nami nitakipindua kiti cha enzi cha falme, nami nitaziharibu nguvu za falme za mataifa; nami nitayapindua magari, na hao wapandao ndani yake; farasi na hao wawapandao wataanguka chini; kila mtu kwa upanga wa ndugu yake. 23 Katika siku ile, asema Bwana wa majeshi, nitakutwaa wewe, Ee Zerubabeli, mtumishi wangu, mwana wa Shealtieli, asema Bwana, nami nitakufanya kuwa kama pete yenye muhuri; kwa kuwa nimekuchagua, asema Bwana wa majeshi.

Zekaria 1

1 Katika mwezi wa nane, mwaka wa pili wa Dario, neno la Bwana lilimjia Zekaria, mwana wa Berekia, mwana wa Ido, nabii, kusema, 2 Bwana amewakasirikia sana baba zenu. 3 Basi, uwaambie, Bwana wa majeshi asema hivi, Nirudieni mimi, asema Bwana wa majeshi, nami nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi. 4 Msiwe ninyi kama baba zenu, ambao manabii wa zamani waliwalilia, wakisema, Bwana wa majeshi asema hivi, Rudini sasa, na kuziacha njia zenu mbovu, na matendo yenu maovu; lakini hawakusikia, wala kunisikiliza, asema Bwana. 5 Je! Baba zenu wako wapi? Nao manabii je! Waishi milele? 6 Lakini maneno yangu, na amri zangu nilizowaagiza hao manabii, watumishi wangu, je! Hazikuwapata baba zenu? Nao wakageuka na kusema, Vile vile kama Bwana wa majeshi alivyoazimia kututenda, sawasawa na njia zetu, na sawasawa na matendo yetu, ndivyo alivyotutenda. 7 Siku ya ishirini na nne ya mwezi wa kumi na moja, yaani, mwezi uitwao Shebati, katika mwaka wa pili wa Dario, neno la Bwana lilimjia Zekaria, mwana wa Berekia, mwana wa Ido, nabii, kusema, 8 Naliona wakati wa usiku, na tazama, mtu amepanda farasi mwekundu, akasimama kati ya mihadasi iliyokuwa mahali penye uvuli; na nyuma yake walikuwapo farasi wengine wekundu, na wa rangi ya kijivujivu, na weupe. 9 Ndipo nikasema, Ee Bwana wangu, ni nini hawa? Basi yule malaika aliyesema nami akaniambia, Nitakuonyesha ni nini hawa. 10 Na yule mtu aliyesimama kati ya mihadasi akajibu, akasema, Hawa ndio Bwana aliowatuma, waende huko na huko duniani. 11 Nao wakamjibu yule malaika wa Bwana aliyesimama kati ya mihadasi, wakasema, Tumekwenda huko na huko duniani, na tazama, dunia yote inatulia, nayo imestarehe. 12 Ndipo yule malaika wa Bwana akajibu, akasema, Ee Bwana wa majeshi, hata lini utakataa kuurehemu Yerusalemu, na miji ya Yuda uliyoikasirikia miaka hii sabini? 13 Naye Bwana akamjibu yule malaika aliyesema nami kwa maneno mazuri, maneno yenye faraja. 14 Basi yule malaika aliyesema nami akaniambia, Haya, piga kelele na kusema, Bwana wa majeshi asema hivi, Naona wivu kwa ajili ya Yerusalemu, na kwa ajili ya Sayuni; naona wivu mkuu sana. 15 Nami ninawakasirikia sana mataifa wanaokaa hali ya raha; kwa maana mimi sikukasirika ila kidogo tu, na wao waliyahimiza mateso. 16 Kwa sababu hiyo Bwana asema hivi, Ninaurudia Yerusalemu kwa rehema nyingi; nyumba yangu itajengwa ndani yake, asema Bwana wa majeshi, na kamba itanyoshwa juu ya Yerusalemu. 17 Piga kelele tena, na kusema, Bwana wa majeshi asema hivi, Miji yangu kwa kufanikiwa itaenezwa huko na huko tena; naye Bwana ataufariji Sayuni tena, atauchagua Yerusalemu tena. 18 Nami nikainua macho yangu, nikaona, na tazama, pembe nne. 19 Nami nikamwuliza yule malaika aliyesema nami, Nini hizi? Naye akanijibu, Hizi ndizo pembe zilizowatawanya watu wa Yuda, na Israeli, na Yerusalemu. 20 Kisha Bwana akanionyesha wafua chuma wanne. 21 Ndipo nikauliza Hawa wanakuja kufanya nini? Akasema kwamba, Hizi ndizo pembe zilizowatawanya watu wa Yuda, hata ikawa hakuna mtu aliyeinua kichwa chake; lakini hawa wamekuja kuzifukuza, kuziangusha pembe za mataifa, walioinua pembe yao juu ya nchi ya Yuda, ili kuwatawanya watu wake.

Zekaria 2

1 Kisha nikainua macho yangu, nikaona, na tazama, mtu mwenye kamba ya kupimia mkononi mwake. 2 Ndipo nikasema, Unakwenda wapi? Akaniambia, Ninakwenda kuupima Yerusalemu, nione upana wake ulivyo na urefu wake ulivyo. 3 Na tazama, yule malaika aliyesema nami akasimama karibu, na malaika mwingine akatoka ili kuonana naye; 4 naye akamwambia, Piga mbio, kamwambie kijana huyu, na kusema, Yerusalemu utakaliwa na watu, kama vijiji visivyo na kuta, kwa sababu ya wingi wa watu na mifugo iliyomo ndani yake. 5 Kwa maana mimi, asema Bwana, nitakuwa ukuta wa moto kuuzunguka pande zote, nami nitakuwa huo utukufu ndani yake. 6 Haya! Haya! Ikimbieni nchi ya kaskazini, asema Bwana; kwa maana mimi nimewatawanya ninyi kama pepo nne za mbinguni, asema Bwana. 7 Haya! Ee Sayuni, jiponye, wewe ukaaye pamoja na binti Babeli. 8 Kwa maana Bwana wa majeshi asema hivi, Ili nitafute utukufu amenituma kwa mataifa wale waliowateka ninyi; maana yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho lake. 9 Kwa maana, tazama, nitatikisa mkono wangu juu yao, nao watakuwa mateka ya hao waliowatumikia; nanyi mtajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma. 10 Imba, ufurahi, Ee binti Sayuni; maana, tazama, ninakuja, nami nitakaa kati yako, asema Bwana. 11 Na mataifa mengi watajiunga na Bwana katika siku ile, nao watakuwa watu wangu; nami nitakaa kati yako, nawe utajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma kwako. 12 Na Bwana atairithi Yuda, iwe sehemu yake katika nchi takatifu, naye atachagua Yerusalemu tena. 13 Nyamazeni, ninyi nyote wenye mwili, mbele za Bwana; kwa maana ameamka, na kutoka katika maskani yake takatifu.

Zekaria 3

1 Kisha akanionyesha Yoshua, kuhani mkuu, amesimama mbele ya malaika wa Bwana, na Shetani amesimama mkono wake wa kuume ili kushindana naye. 2 Bwana akamwambia Shetani, Bwana na akukemee Ewe Shetani; naam, Bwana, aliyechagua Yerusalemu, na akukemee; je! Hiki si kinga kilichotolewa motoni? 3 Basi, Yoshua alikuwa amevaa nguo chafu sana, naye alikuwa akisimama mbele ya malaika. 4 Naye huyo akajibu, akawaambia wale waliosimama mbele yake, akisema, Mvueni nguo hizi zenye uchafu. Kisha akamwambia yeye, Tazama, nimekuondolea uovu wako, nami nitakuvika mavazi ya thamani nyingi. 5 Nikasema, Na wampige kilemba kizuri kichwani pake. Basi, wakampiga kilemba kizuri kichwani pake, wakamvika mavazi; naye malaika wa Bwana akasimama karibu. 6 Kisha malaika wa Bwana akamshuhudia Yoshua, akisema, 7 Bwana wa majeshi asema hivi, Kama ukienda katika njia zangu, na kama ukishika maagizo yangu, ndipo utakapoihukumu nyumba yangu, nawe utazilinda nyua zangu, nami nitakupa nafasi ya kunikaribia kati yao wasimamao karibu. 8 Sikiliza sasa, Ee Yoshua, kuhani mkuu, wewe na wenzako waketio mbele yako; maana hao ni watu walio ishara; kwa maana, tazama, ninamleta mtumishi wangu, aitwaye Chipukizi. 9 Maana, litazame jiwe hili nililoliweka mbele ya Yoshua; katika jiwe moja yako macho saba; tazama, nitachora machoro yake, asema Bwana wa majeshi, nami nitauondoa uovu wa nchi ile katika siku moja. 10 Katika siku ile, asema Bwana wa majeshi, ninyi mtamwalika kila mtu jirani yake chini ya mzabibu, na chini ya mtini.

Zekaria 4

1 Na yule malaika aliyesema nami akanijia mara ya pili, akaniamsha, kama mtu aamshwavyo katika usingizi wake. 2 Akaniuliza, Unaona nini? Nikasema, Nimeona, na tazama, kinara cha taa cha dhahabu tupu, nacho kina bakuli juu yake, na taa zake saba juu yake; tena iko mirija saba ya kuleta mafuta, kwa taa zote zilizo juu yake; 3 na mizeituni miwili karibu yake, mmoja upande wa kuume walile bakuli, na mmoja upande wake wa kushoto. 4 Nami nikajibu, nikamwambia yule malaika aliyesema nami, nikasema, Ee Bwana wangu, vitu hivi ni nini? 5 Ndipo malaika aliyesema nami akajibu, akaniambia, Hujui vitu hivi ni nini? Nikasema, La, Bwana wangu. 6 Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi. 7 Nani wewe, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli utakuwa nchi tambarare; naye atalileta lile jiwe la kuwekwa juu kabisa pamoja na vigelegele vya, Neema, neema, ilikalie. 8 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, 9 Mikono yake Zerubabeli imeiweka misingi ya nyumba hii, na mikono yake ndiyo itakayoimaliza; nawe utajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma kwenu. 10 Maana ni nani aliyeidharau siku ya mambo madogo? Kwa kuwa watafurahi, nao wataiona timazi katika mkono wa Zerubabeli; naam, hizi saba ndizo macho ya Bwana; yapiga mbio huko na huko duniani mwote. 11 Ndipo nikajibu, nikamwambia, Ni nini mizeituni hii miwili iliyo upande wa kuume wa kinara cha taa kile na upande wake wa kushoto? 12 Nami nikajibu mara ya pili, nikamwuliza, Ni nini haya matawi mawili ya mizeituni, ambayo kwa njia ya ile mifereji miwili ya dhahabu hutoa mafuta yao? 13 Akanijibu, akasema, Hujui hivi ni nini? Nikasema, La, Bwana wangu. 14 Ndipo akasema, Hivi ni hao wana wawili wa mafuta, wasimamao karibu na Bwana wa dunia yote.

Zekaria 5

1 Basi, nikainua macho yangu tena, nikaona, na tazama, gombo la chuo lirukalo. 2 Akaniuliza, Unaona nini? Nikajibu, Naona gombo la chuo lirukalo; na urefu wake ni dhiraa ishirini, na upana wake dhiraa kumi. 3 Ndipo akaniambia, Hii ndiyo laana itokayo kwenda juu ya uso wa nchi yote; maana kwa hiyo kila aibaye atatolewa kama ilivyo upande mmoja, na kwa hiyo kila aapaye atatolewa kama ilivyo upande wa pili. 4 Nitaituma itokee, asema Bwana wa majeshi, nayo itaingia katika nyumba ya mwivi, na katika nyumba yake yeye aapaye kwa uongo kwa jina langu; nayo itakaa katikati ya nyumba yake, na kuiteketeza, pamoja na boriti zake na mawe yake. 5 Ndipo yule malaika aliyesema nami akatokea, akaniambia, Inua macho yako sasa, uone ni kitu gani kitokeacho. 6 Nikasema, Ni kitu gani? Akasema, Kitu hiki ni efa itokeayo. Tena akasema, Huu ndio uovu wao katika nchi hii yote; 7 na tazama, talanta ya risasi iliinuliwa; na tazama, mwanamke akaaye katikati ya hiyo efa. 8 Akasema, Huyu ni Uovu; akamtupa chini katikati ya ile efa; akalitupa lile jiwe la risasi juu ya mdomo wa ile efa. 9 Ndipo nikainua macho yangu, nikaona, na tazama, wanawake wawili walitokea, nao upepo ulikuwa katika mabawa yao; na mabawa yao yalikuwa kama mabawa ya korongo; wakaiinua ile efa kati ya dunia na mbingu. 10 Ndipo nikamwambia yule malaika aliyesema nami, Hawa wanaipeleka wapi efa hii? 11 Akaniambia, Wanakwenda kumjengea nyumba katika nchi ya Shinari; tena ikiisha kutengenezwa, atawekwa huko mahali pake mwenyewe.

Zekaria 6

1 Nikainua macho yangu tena, nikaona, na tazama, yanatokea magari ya vita manne, yanatoka kati ya milima miwili, na milima hiyo ilikuwa ni milima ya shaba. 2 Katika gari la kwanza walikuwa farasi wekundu; na katika gari la pili walikuwa farasi weusi; 3 na katika gari la tatu walikuwa farasi weupe; na katika gari la nne walikuwa farasi wa rangi ya kijivujivu. 4 Nikajibu, nikamwuliza yule malaika aliyesema nami, Hawa ni nini, Bwana wangu? 5 Malaika akajibu, akaniambia, Hawa ni pepo nne za mbinguni, zitokeazo baada ya kusimama mbele za Bwana wa dunia yote. 6 Gari lile lenye farasi weusi latoka kwenda hata nchi ya kaskazini; nao farasi weupe wakatoka wakafuata nyuma yao; na wale wa rangi ya kijivujivu wakatoka kwenda hata nchi ya kusini. 7 Na wale wekundu wakatoka, wakataka kwenda huko na huko katika dunia; naye akawaambia, Haya! Tokeni, mwende huko na huko katika dunia. Basi wakaenda huko na huko katika dunia. 8 Ndipo akaniita, akaniambia akisema, Tazama, wale waendao mpaka nchi ya kaskazini wameituliza roho yangu katika nchi ya kaskazini. 9 Neno la Bwana likanijia, kusema, 10 Pokea vitu mikononi mwa baadhi ya watu waliohamishwa, yaani, Heldai, na Tobia, na Yedaya; na siku iyo hiyo enenda ukaingie katika nyumba ya Yosia, mwana wa Sefania, waliyoifikia kutoka Babeli; 11 naam, pokea fedha na dhahabu, ukafanye taji, ukamvike kichwani Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu; 12 ukamwambie, ukisema, Bwana wa majeshi asema hivi, ya kwamba, Tazama, mtu huyu ndiye ambaye jina lake ni Chipukizi; naye atakua katika mahali pake, naye atalijenga hekalu la Bwana. 13 Naam, yeye atalijenga hekalu la Bwana; naye atauchukua huo utukufu; ataketi akimiliki katika kiti chake cha enzi; na kutakuwa na kuhani katika kiti chake cha enzi; na shauri la amani litakuwa kati ya hao wawili. 14 Na hizo taji zitakuwa za Heldai, na Tobia, na Yedaya; na kwa fadhili za mwana wa Sefania; ziwe ukumbusho katika hekalu la Bwana. 15 Nao walio mbali watakuja na kujenga katika hekalu la Bwana, nanyi mtajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma kwenu. Na haya yatatokea, kama mkijitahidi kuitii sauti ya Bwana, Mungu wenu.

Zekaria 7

1 Ikawa katika mwaka wa nne wa mfalme Dario, neno la Bwana lilimjia Zekaria, siku ya nne ya mwezi wa kenda, yaani, Kisleu. 2 Basi watu wa Betheli walikuwa wamewatuma Shareza na Regem-meleki, na watu wao, ili kuomba fadhili za Bwana, 3 na kusema na makuhani wa nyumba ya Bwana wa majeshi, na hao manabii, ya kwamba, Je! Yanipasa kulia katika mwezi wa tano, na kujitenga na watu, kama nilivyofanya miaka hii mingi iliyopita? 4 Ndipo neno la Bwana wa majeshi likanijia, kusema, 5 Waambie watu wote wa nchi, na hao makuhani, ukisema, Hapo mlipofunga na kuomboleza katika mwezi wa tano na mwezi wa saba, katika miaka hiyo sabini, je! Mlinifungia mimi kwa lo lote; mlinifungia mimi? 6 Na wakati mlapo chakula na kunywa, je! Hamli kwa ajili ya nafsi zenu, na kunywa kwa ajili ya nafsi zenu? 7 Je! Hayo siyo maneno aliyoyasema Bwana kwa vinywa vya manabii wa zamani, wakati Yerusalemu ulipokaliwa na watu na kufanikiwa, na miji yake iliyokuwa ikiuzunguka; na wakati ule ambao nchi ya Negebu na Shefela ilipokuwa ikikaliwa na watu? 8 Kisha neno la Bwana likamjia Zekaria, kusema, 9 Bwana wa majeshi amesema hivi, ya kwamba, Fanyeni hukumu za kweli, kila mtu na amwonee ndugu yake rehema na huruma; 10 tena msimdhulumu mjane, wala yatima, wala mgeni, wala maskini; wala mtu awaye yote miongoni mwenu asiwaze mabaya juu ya ndugu yake moyoni mwake. 11 Lakini hao walikataa kusikiliza, wakageuza bega lao, wakaziba masikio yao ili wasisikie. 12 Naam, walifanya mioyo yao kuwa kama jiwe gumu, wasije wakaisikia sheria na maneno ya Bwana wa majeshi, aliyoyapeleka kwa roho yake kwa mkono wa manabii wa kwanza; kwa sababu hiyo ghadhabu kuu ikatoka kwa Bwana wa majeshi. 13 Ikawa kwa sababu alilia, wao wasitake kusikiliza; basi, wao nao watalia, wala mimi sitasikiliza, asema Bwana wa majeshi. 14 Lakini nitawatawanya kwa upepo wa kisulisuli, katikati ya mataifa yote wasiowajua. Basi hivyo ndivyo ilivyokuwa ukiwa nchi baada yao, hata hapakuwa na mtu aliyepita kati yake, wala aliyerudi; maana waliifanya nchi iliyopendeza sana kuwa ukiwa.

Zekaria 8

1 Neno la Bwana wa majeshi likanijia, kusema, 2 Bwana wa majeshi asema hivi, Mimi nina wivu kwa ajili ya Sayuni, wivu mkuu, nami nina wivu kwa ajili yake kwa ghadhabu kuu. 3 Bwana asema hivi, Mimi nimerudi Sayuni, nami nitakaa katikati ya Yerusalemu; na Yerusalemu utaitwa, Mji wa kweli; na Mlima wa Bwana wa majeshi utaitwa, Mlima mtakatifu. 4 Bwana wa majeshi asema hivi, Wazee wanaume na wazee wanawake watakaa tena katika njia za Yerusalemu, kila mtu ana mkongojo wake mkononi, kwa kuwa ni mzee sana. 5 Na hizo njia za mji zitajaa wavulana, na wasichana, wakicheza katika njia zake. 6 Bwana wa majeshi asema hivi, Ingawa hili ni neno lililo gumu mbele ya macho ya mabaki ya watu hawa katika siku hizo, je! Liwe neno gumu mbele ya macho yangu? Asema Bwana wa majeshi. 7 Bwana wa majeshi asema hivi, Tazama, nitawaokoa watu wangu toka nchi ya mashariki, na toka nchi ya magharibi; 8 nami nitawaleta, nao watakaa katikati ya Yerusalemu; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao, katika kweli na katika haki. 9 Bwana wa majeshi asema hivi, Mikono yenu na iwe hodari, ninyi mnaosikia siku hizi maneno haya kwa vinywa vya manabii, waliokuwapo siku hiyo ulipowekwa msingi wa nyumba ya Bwana wa majeshi; yaani, hekalu hilo; ili lijengwe. 10 Maana kabla ya siku zile hapakuwa na ijara kwa mwanadamu, wala hapakuwa na ijara kwa mnyama; wala hapakuwa na amani kwake yeye aliyetoka, wala kwake yeye aliyeingia, kwa sababu ya adui; nami nalimwacha kila mtu kugombana na jirani yake. 11 Lakini sasa sitakuwa kwa mabaki ya watu hawa kama nilivyokuwa siku zile za kwanza, asema Bwana wa majeshi. 12 Kwa maana itakuwako mbegu ya amani; mzabibu utatoa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, na hizo mbingu zitatoa umande wake; nami nitawarithisha mabaki ya watu hawa vitu hivi vyote. 13 Kisha itakuwa, kama vile mlivyokuwa laana katika mataifa, Ee nyumba ya Yuda, na nyumba ya Israeli, ndivyo nitakavyowaokoa, nanyi mtakuwa baraka; msiogope, lakini mikono yenu na iwe hodari. 14 Maana Bwana wa majeshi asema hivi, Kama vile nilivyoazimia kuwatenda ninyi mabaya, baba zenu waliponikasirisha, asema Bwana wa majeshi, wala mimi sikujuta; 15 vivyo hivyo nimeazimia katika siku hizi kuutendea Yerusalemu mema, na nyumba ya Yuda pia; msiogope. 16 Haya ndiyo mtakayoyatenda; kila mtu na aseme kweli na jirani yake; hukumuni kweli na hukumu ya amani malangoni mwenu; 17 wala mtu wa kwenu asiwaze mabaya moyoni mwake juu ya jirani yake; wala msipende kiapo cha uongo; maana hayo yote ndiyo niyachukiayo, asema Bwana. 18 Tena neno la Bwana wa majeshi likanijia, kusema, 19 Bwana wa majeshi asema hivi, Saumu ya mwezi wa nne, na saumu ya mwezi wa tano, na saumu ya mwezi wa saba, na saumu ya mwezi wa kumi, zitakuwa furaha na shangwe, na sikukuu za kuchangamkia, kwa nyumba ya Yuda; basi zipendeni kweli na amani. 20 Bwana wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; 21 wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! Twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za Bwana, na kumtafuta Bwana wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. 22 Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta Bwana wa majeshi, na kuomba fadhili za Bwana. 23 Bwana wa majeshi asema hivi, Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.

Zekaria 9

1 Ufunuo wa neno la Bwana, lililosemwa juu ya nchi ya Hadraki, na Dameski itakuwa mahali pake pa kustarehe; kwa maana jicho la mwanadamu na la kabila zote za Israeli linamwelekea Bwana; 2 na Hamathi pia iliyo mpakani mwake; na Tiro, na Sidoni, kwa maana ana akili nyingi. 3 Na Tiro alijijengea ngome, akakusanya fedha kama mchanga, dhahabu safi kama matope ya njia kuu. 4 Tazama, Bwana atamwondolea mali zake, naye ataupiga uwezo wake alio nao baharini, naye mwenyewe atateketezwa kwa moto. 5 Ashkeloni ataona haya na kuogopa; Gaza pia, naye atafadhaika sana; na Ekroni, kwa maana taraja lake litatahayarika; na mfalme ataangamia toka Gaza, na Ashkeloni atakuwa hana watu. 6 Na mwana wa haramu atatawala huko Ashdodi, nami nitakatilia mbali kiburi cha Wafilisti. 7 Nami nitaondoa damu yake kinywani mwake, na machukizo yake nitayatoa katika meno yake; yeye naye atakuwa ni mabaki kwa Mungu wetu; naye atakuwa kama mtu mkuu katika Yuda, na Ekroni kama Myebusi. 8 Nami nitapiga kambi yangu pande zote za nyumba yangu ili kuwapinga adui, mtu awaye yote asipite ndani yake wala kurudi; wala mtu aoneaye hatapita tena kati yao; kwa maana sasa nimeona kwa macho yangu. 9 Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda. 10 Na gari la vita nitaliondoa liwe mbali na Efraimu, na farasi awe mbali na Yerusalemu, na upinde wa vita utaondolewa mbali; naye atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto hata miisho ya dunia. 11 Na kwa habari zako wewe, kwa sababu ya damu ya agano lako, nimewatoa wafungwa wako katika shimo lile lisilo na maji. 12 Irudieni ngome, enyi wafungwa wa tumaini; hata hivi leo nasema ya kwamba nitakurudishia maradufu. 13 Maana nimejipindia Yuda, nimeujaza upinde wangu Efraimu; nami nitawaondokesha wana wako, Ee Sayuni, wapigane na wana wako, Ee Uyunani, nami nitakufanya wewe kuwa kama upanga wa shujaa. 14 Naye Bwana ataonekana juu yao, Na mshale wake utatoka kama umeme; Na Bwana MUNGU ataipiga tarumbeta, Naye atakwenda kwa pepo za kisulisuli za kusini. 15 Bwana wa majeshi atawalinda; Nao watakula na kuyakanyaga mawe ya teo; Nao watakunywa na kufanya kelele kama kwa divai; Nao watajazwa kama mabakuli, kama pembe za madhabahu. 16 Na Bwana, Mungu wao, atawaokoa siku hiyo, Kama kundi la watu wake; Kwa maana watakuwa kama vito vya taji, Vikimeta-meta juu ya nchi yake. 17 Maana wema wake, jinsi ulivyo mwingi! Na uzuri wake, jinsi ulivyo mwingi! Nafaka itawasitawisha vijana wanaume, Na divai mpya vijana wanawake.

Zekaria 10

1 Mwombeni Bwana mvua wakati wa masika, naam, Bwana afanyaye umeme, naye atawapa manyunyu ya mvua, kila mtu atapewa nyasi kondeni. 2 Kwa maana vinyago vimenena maneno ya ubatili, nao waaguzi wameona uongo; nao wameleta habari za ndoto za uongo, wafariji bure; kwa sababu hiyo waenda zao kama kondoo, wateswa, kwa sababu hapana mchungaji. 3 Hasira yangu imewaka juu ya wachungaji, nami nitawaadhibu mbuzi waume; kwa maana Bwana wa majeshi ameliangalia kundi lake, yaani, nyumba ya Yuda, naye atawafanya kuwa kama farasi wake mzuri vitani. 4 Kwake yeye litatoka lile jiwe la pembeni, kwake yeye utatoka msumari, kwake yeye utatoka upinde wa vita, kwake yeye atatoka kila mtawala pamoja. 5 Nao watakuwa kama mashujaa, wakanyagao adui zao katika matope ya njia vitani; nao watapiga vita, kwa sababu Bwana yu pamoja nao; na hao wapandao farasi watafadhaishwa. 6 Nami nitaitia nguvu nyumba ya Yuda, nami nitaiokoa nyumba ya Yusufu, nami nitawarudisha, kwa maana nawaonea rehema; nao watakuwa kana kwamba sikuwatupa; kwa maana mimi ni Bwana, Mungu wao, nami nitawasikia. 7 Na watu wa Efraimu watakuwa kama shujaa, na moyo wao utafurahi kana kwamba ni kwa divai; naam, watoto wao wataona mambo haya, na kufurahi; mioyo yao itamfurahia Bwana. 8 Nitawapigia kelele, na kuwakusanya pamoja; kwa maana nimewakomboa; nao wataongezeka kama walivyoongezeka. 9 Nami nitawapanda kama mbegu kati ya mataifa; nao watanikumbuka katika nchi zilizo mbali; nao watakaa pamoja na watoto wao; tena watarudi. 10 Tena nitawarudisha toka nchi ya Misri, nitawakusanya na kuwatoa katika Ashuru; nami nitawaingiza katika nchi ya Gileadi na Lebanoni; ila nafasi ya kuwatosha haitaonekana. 11 Naye atapita kati ya bahari ya mateso, na kuyapiga mawimbi ya bahari, na vilindi vyote vya mto wa Nile vitakauka; na kiburi cha Ashuru kitashushwa; na fimbo ya enzi ya Misri itatoweka. 12 Nami nitawatia nguvu katika Bwana; nao watatembea huko na huko katika jina lake, asema Bwana.

Zekaria 11

1 Ifungue milango yako, Ee Lebanoni, Ili moto uiteketeze mierezi yako. 2 Piga yowe, msunobari, maana mwerezi umeanguka, Kwa sababu miti iliyo mizuri imeharibika; Pigeni yowe, enyi mialoni ya Bashani, Kwa maana msitu wenye nguvu umeangamia. 3 Sauti ya wachungaji, ya uchungu mwingi! Kwa maana utukufu wao umeharibika; Sauti ya ngurumo ya wana-simba! Kwa maana kiburi cha Yordani kimeharibika. 4 Bwana, Mungu wangu, alisema hivi, Lilishe kundi la machinjo, 5 ambalo wenye kundi hilo huwachinja, kisha hujiona kuwa hawana hatia; na hao wawauzao husema, Na ahimidiwe Bwana, kwa maana mimi ni tajiri; na wachungaji wao wenyewe hawawahurumii. 6 Maana mimi sitawahurumia tena wenyeji wa nchi hii, asema Bwana; bali, tazama, nitawatia, kila mmoja wao, mikononi mwa mwenzake, na mikononi mwa mfalme; nao wataipiga hiyo nchi, wala mimi sitawaokoa mikononi mwao. 7 Basi nikalilisha kundi la machinjo, kweli kondoo waliokuwa wanyonge kabisa. 8 Nami nikawakatilia mbali wachungaji watatu katika mwezi mmoja; maana nafsi yangu ilikuwa imechoka kwa ajili yao, na nafsi zao pia walinichukia. 9 Ndipo nikasema, Sitawalisheni; afaye na afe; atakayekatiliwa mbali na akatiliwe mbali; nao waliosalia, kila mmoja na ale nyama ya mwili wa mwenziwe. 10 Nikaitwaa hiyo fimbo yangu, iitwayo Neema, nikaikata vipande viwili, ili nipate kulivunja agano langu nililolifanya na watu wa kabila zote. 11 Nayo ikavunjwa siku ile; na hivyo wale kondoo wanyonge walionisikiliza wakajua ya kuwa neno hili ndilo neno la Bwana. 12 Nikawaambia, Mkiona vema, nipeni ujira wangu; kama sivyo, msinipe. Basi wakanipimia vipande thelathini vya fedha, kuwa ndio ujira wangu. 13 Kisha Bwana akaniambia, Mtupie mfinyanzi kima kizuri, hicho nilichotiwa kima na watu hao. Basi nikavitwaa vile vipande thelathini vya fedha, nikamtupia huyo mfinyanzi ndani ya nyumba ya Bwana. 14 Ndipo nikaikata vipande viwili fimbo yangu ya pili, iitwayo Vifungo, ili nipate kuuvunja udugu uliokuwa kati ya Yuda na Israeli. 15 Bwana akaniambia, Jitwalie tena vyombo vya mchungaji mpumbavu. 16 Kwa maana, tazama, mimi nitainua katika nchi hii mchungaji, ambaye hatawaangalia waliopotea, wala hatawatafuta waliotawanyika, wala hatamganga aliyevunjika, wala hatamlisha aliye mzima; bali atakula nyama ya wanono, na kuzirarua-rarua kwato zao. 17 Ole wake mchungaji asiyefaa, aliachaye kundi! Upanga utakuwa juu ya mkono wake, na juu ya jicho lake la kuume; mkono wake utakuwa umekauka kabisa, na jicho lake la kuume litakuwa limepofuka.

Zekaria 12

1 Ufunuo wa neno la Bwana juu ya Israeli. Haya ndiyo asemayo Bwana, azitandaye mbingu, auwekaye msingi wa dunia, aiumbaye roho ya mwanadamu ndani yake. 2 Angalia, mimi nitafanya Yerusalemu kuwa kikombe cha kuyumba-yumba kwa watu wa kabila zote, wazungukao pande zote; tena kitakuwa juu ya Yuda pia wakati wa kuhusuriwa Yerusalemu. 3 Tena itakuwa siku hiyo, nitafanya Yerusalemu kuwa jiwe la kuwalemea watu wa kabila zote; wote watakaojitwika jiwe hilo watapata jeraha nyingi; na mataifa yote ya dunia watakusanyika pamoja juu yake. 4 Katika siku hiyo, asema Bwana, nitamtia kila farasi ushangao, na yeye ampandaye nitamtia wazimu; nami nitaifunulia nyumba ya Yuda macho yangu, nami nitamtia upofu kila farasi wa hizo kabila za watu. 5 Na wakuu wa Yuda watasema mioyoni mwao, Wenyeji wa Yerusalemu ni nguvu zangu katika Bwana wa majeshi, Mungu wao. 6 Siku hiyo nitawafanya wakuu wa Yuda kuwa kama kigae chenye moto katika kuni, na kama kinga cha moto katika miganda; nao watateketeza watu wa kila kabila, wawazungukao pande zote, upande wa mkono wa kuume na upande wa mkono wa kushoto; na baada ya haya Yerusalemu utakaa mahali pake, naam, hapo Yerusalemu. 7 Naye Bwana ataziokoa hema za Yuda kwanza, ili utukufu wa nyumba ya Daudi, na utukufu wa wenyeji wa Yerusalemu, usipate kutukuzwa kuliko Yuda. 8 Katika siku hiyo Bwana atawalinda wenyeji wa Yerusalemu; na yeye aliye dhaifu miongoni mwao atakuwa kama Daudi siku hiyo; nayo nyumba ya Daudi itakuwa kama Mungu, kama malaika wa Bwana mbele yao. 9 Hata itakuwa siku hiyo, ya kwamba nitatafuta kuwaangamiza mataifa yote watakaokuja kupigana na Yerusalemu. 10 Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao watamtazama yeye ambaye walimchoma; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza. 11 Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makuu huko Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika bonde la Megido. 12 Nayo nchi itaomboleza, kila jamaa peke yake; jamaa ya nyumba ya Daudi peke yao, na wake zao peke yao; jamaa ya nyumba ya Nathani peke yao, na wake zao peke yao; 13 jamaa ya nyumba ya Lawi peke yao, na wake zao peke yao; jamaa ya nyumba ya Shimei peke yao, na wake zao peke yao. 14 Jamaa zote zilizosalia, kila jamaa peke yake, na wake zao peke yao.

Zekaria 13

1 Katika siku hiyo watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, watafunguliwa chemchemi kwa dhambi na kwa unajisi. 2 Kisha itakuwa katika siku hiyo, asema Bwana wa majeshi, nitakatilia mbali majina ya sanamu katika nchi, yasikumbukwe tena; pia nitawafukuza manabii, na roho ya uchafu, watoke katika nchi. 3 Tena itakuwa ya kwamba, mtu awaye yote atakapotoa unabii, basi baba yake na mama yake waliomzaa watamwambia, Hutaishi; kwa maana unanena maneno ya uongo kwa jina la Bwana; na baba yake na mama yake waliomzaa watamtumbua atoapo unabii. 4 Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba manabii, kila mmoja wao, atayaonea haya maono yake atoapo unabii; wala hawatavaa joho ya nywele ili kudanganya watu; 5 bali atasema, Mimi si nabii kamwe; mimi ni mkulima wa nchi; kwa maana nalifanywa mtumwa tokea ujana wangu. 6 Na mtu atamwambia, Je! Jeraha hizi ulizo nazo kati ya mikono yako ni nini? Naye atajibu, Ni jeraha nilizotiwa katika nyumba ya rafiki zangu. 7 Amka, Ee upanga, juu ya mchungaji wangu, na juu ya mtu aliye mwenzangu, asema Bwana wa majeshi; mpige mchungaji, nao kondoo watatawanyika; nami nitaugeuza mkono wangu juu ya wadogo. 8 Hata itakuwa, ya kwamba katika nchi yote mafungu mawili yatakatiliwa mbali, nao watakufa, asema Bwana; lakini fungu la tatu litabaki humo. 9 Nami nitalileta fungu lile la tatu na kulipitisha kati ya moto, nami nitawasafisha kama fedha isafishwavyo, nami nitawajaribu kama dhahabu ijaribiwavyo; wataliitia jina langu, nami nitawasikia; mimi nitasema, Watu hawa ndio wangu; nao watasema, Bwana ndiye Mungu wangu.

Zekaria 14

1 Tazama, siku moja ya Bwana inakuja, ambayo mateka yatagawanyika kati yako. 2 Kwa maana nitawakusanya mataifa yote walete vita juu ya Yerusalemu; na huo mji utapigwa, nazo nyumba zitatekwa, nao wanawake watatendwa jeuri; na nusu ya watu wa mji watatoka kwenda utumwani; ila mabaki ya watu wa mji hawatakatiliwa mbali. 3 Hapo ndipo atakapotokea Bwana, naye atapigana na mataifa hayo, kama vile alipopigana zamani siku ya vita. 4 Na siku hiyo miguu yake itasimama juu ya mlima wa Mizeituni, unaoelekea Yerusalemu upande wa mashariki, nao mlima wa Mizeituni utapasuka katikati yake, upande wa mashariki na upande wa magharibi; litakuwako huko bonde kubwa sana; na nusu ya mlima ule utaondoka kwenda upande wa kaskazini, na nusu yake itaondoka kwenda upande wa kusini. 5 Nanyi mtakimbia kwa njia ya bonde la milima yangu; kwa maana bonde lile la milima litaenea hata Aseli; naam, mtakimbia, kama vile mlivyokimbia mbele ya tetemeko la nchi, siku za Uzia, mfalme wa Yuda; na Bwana, Mungu wangu, atakuja, na watakatifu wote pamoja naye. 6 Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba nuru yake haitakuwa na mwangaza na kiwi; 7 lakini itakuwa siku moja, iliyojulikana na Bwana; si mchana, wala si usiku; lakini itakuwa, ya kwamba wakati wa jioni kutakuwako nuru. 8 Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba maji yaliyo hai yatatoka katika Yerusalemu; nusu yake itakwenda upande wa bahari ya mashariki, na nusu yake upande wa bahari ya magharibi; wakati wa hari na wakati wa baridi itakuwa hivi. 9 Naye Bwana atakuwa Mfalme juu ya nchi yote; siku hiyo Bwana atakuwa mmoja, na jina lake moja. 10 Nchi yote itageuzwa kuwa kama Araba, toka Geba mpaka Rimoni upande wa kusini wa Yerusalemu; naye atainuliwa juu, atakaa mahali pake mwenyewe, toka lango la Benyamini mpaka mahali pa lango la kwanza, mpaka lango la pembeni; tena toka mnara wa Hananeli mpaka mashinikizo ya mfalme. 11 Na watu watakaa ndani yake, wala hakutakuwako laana tena; lakini Yerusalemu utakaa salama. 12 Na hii ndiyo tauni, ambayo Bwana atawapiga watu wote waliofanya vita juu ya Yerusalemu; nyama ya mwili wao itaharibika, wasimamapo juu ya miguu yao, na macho yao yataharibika ndani ya vichwa vyao, na ndimi zao zitaharibika vinywani mwao. 13 Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba mashaka makubwa yatokayo kwa Bwana yatakuwa kati yao; na kila mmoja wao atakamata mkono wa jirani yake, na mkono wake utainuliwa ili kushindana na mkono wa jirani yake. 14 Yuda naye atafanya vita juu ya Yerusalemu; na huo utajiri wa mataifa wa pande zote utakusanyika, dhahabu, na fedha, na mavazi; vitu vingi sana. 15 Na hivyo ndivyo itakavyokuwa tauni ya farasi, na nyumbu, na ngamia, na punda, na ya hao wanyama wote watakaokuwamo matuoni mle, kama tauni hiyo. 16 Hata itakuwa, ya kwamba kila mtu aliyesalia wa mataifa yote, waliokuja kupigana na Yerusalemu, atakwea mwaka baada ya mwaka ili kumwabudu Mfalme, Bwana wa majeshi, na kuishika sikukuu ya Vibanda. 17 Tena itakuwa, ya kwamba mtu awaye yote wa jamaa zote zilizomo duniani, asiyekwea kwenda Yerusalemu ili kumwabudu Mfalme, Bwana wa majeshi, mvua haitanyesha kwao. 18 Na kama jamaa ya Misri hawakwei, wala hawaji, pia haitanyesha kwao; itakuwako tauni, ambayo Bwana atawapiga mataifa, wasiokwea ili kushika sikukuu ya Vibanda. 19 Hii ndiyo adhabu ya Misri, na adhabu ya mataifa yote, wasiokwea ili kushika sikukuu ya Vibanda. 20 Siku hiyo katika njuga za farasi yataandikwa maneno haya, WATAKATIFU KWA Bwana; navyo vyombo vilivyomo ndani ya nyumba ya Bwana vitakuwa kama mabakuli yaliyoko mbele ya madhabahu.

Malaki 1

1 Ufunuo wa neno la Bwana kwa Israeli kwa mkono wa Malaki 2 Nimewapenda ninyi, asema Bwana. Lakini ninyi mwasema, Umetupendaje? Je! Esau siye ndugu yake Yakobo? Asema Bwana; ila nimempenda Yakobo; 3 bali Esau nimemchukia na kuifanya milima yake kuwa ukiwa, na urithi wake nimewapa mbweha wa nyikani. 4 Ijapokuwa Edomu asema, Tumepondwa-pondwa, lakini tutarudi na kupajenga mahali palipoachwa hali ya ukiwa; Bwana wa majeshi asema hivi, Wao watajenga, bali mimi nitaangusha; na watu watawaita, Mpaka wa uovu, na, Watu ambao Bwana anawaghadhabikia milele. 5 Na macho yenu ninyi yataona, nanyi mtasema, Bwana ndiye mkuu kupita mpaka wa Israeli. 6 Mwana humheshimu baba yake, na mtumishi humcha bwana wake; basi, kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? Na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi? Bwana wa majeshi awauliza ninyi, enyi makuhani, mnaolidharau jina langu. Nanyi mwasema, Tumelidharau jina lako kwa jinsi gani? 7 Mnatoa chakula kilichotiwa unajisi juu ya madhabahu yangu Nanyi mwasema, Sisi tumekutia unajisi kwa jinsi gani? Kwa sababu mwasema, Meza ya Bwana ni kitu cha kudharauliwa. 8 Tena mtoapo sadaka aliye kipofu, si vibaya? Na mtoapo sadaka walio vilema na wagonjwa, si vibaya? Haya! Mtolee liwali wako; je! Atakuwa radhi nawe? Au atakukubali nafsi yako? Asema Bwana wa majeshi. 9 Na sasa, nawasihi, ombeni fadhili za Mungu, ili atupe neema; ikiwa jambo hili limetoka katika mikono yenu; je! Atawakubali nafsi zenu? Asema Bwana wa majeshi. 10 Laiti angekuwapo kwenu mtu mmoja wa kuifunga milango; msije mkawasha moto bure madhabahuni pangu! Sina furaha kwenu, asema Bwana wa majeshi, wala sitakubali dhabihu yo yote mikononi mwenu. 11 Kwa maana tokea maawio ya jua hata machweo yake jina langu ni kuu katika Mataifa; na katika kila mahali unatolewa uvumba na dhabihu safi kwa jina langu; maana jina langu ni kuu katika Mataifa, asema Bwana wa majeshi. 12 Lakini ninyi mnalitia unajisi, kwa kuwa mwasema, Meza ya Bwana imetiwa unajisi; na matunda yake, yaani, nyama yake, hudharauliwa. 13 Tena mwasema, Tazama, jambo hili linatuchokesha namna gani! Nanyi mmelidharau, asema Bwana wa majeshi; nanyi mmeleta kitu kilichopatikana kwa udhalimu, na kilema, na kilicho kigonjwa; ndivyo mnavyoleta sadaka; je! Niikubali hii mikononi mwenu? Asema Bwana. 14 Lakini na alaaniwe mtu mwenye kudanganya, ambaye katika kundi lake ana mume, akaweka nadhiri, ila amtolea Bwana kitu kilicho na kilema; kwa maana mimi ni Mfalme mkuu, asema Bwana wa majeshi, na jina langu latisha katika Mataifa.

Malaki 2

1 Na sasa, enyi makuhani, amri hii yawahusu ninyi. 2 Kama hamtaki kusikia, na kama hamtaki kuitia moyoni, ili kulitukuza jina langu, asema Bwana wa majeshi, basi nitawapelekeeni laana, nami nitazilaani baraka zenu; naam, nimekwisha kuzilaani, kwa sababu hamyatii haya moyoni. 3 Angalieni, nitaikemea mbegu kwa ajili yenu, nami nitapaka nyuso zenu mavi, naam, mavi ya sadaka zenu; nanyi mtaondolewa pamoja nayo 4 Nanyi mtajua ya kuwa mimi nimewapelekeeni amri hii, ili agano langu liwe na Lawi, asema Bwana wa majeshi. 5 Agano langu naye lilikuwa agano la uhai na amani; nami nikampa ili aogope, naye akaniogopa, akalicha jina langu. 6 Sheria ya kweli ilikuwa kinywani mwake, wala udhalimu haukuonekana midomoni mwake; alikwenda pamoja nami katika amani na unyofu, na kuwageuza wengi hata wakaacha uovu. 7 Kwa maana yapasa midomo ya kuhani ihifadhi maarifa, tena yawapasa watu kuitafuta sheria kinywani mwake; kwa kuwa yeye ni mjumbe wa Bwana wa majeshi. 8 Bali ninyi mmegeuka mkaiacha njia; mmewakwaza watu wengi katika sheria; mmeliharibu agano la Lawi, asema Bwana wa majeshi. 9 Kwa sababu hiyo mimi nami nimewafanya ninyi kuwa kitu cha kudharauliwa, na unyonge, mbele ya watu wote, kama vile ninyi msivyozishika njia zangu, bali mmewapendelea watu katika sheria. 10 Je! Sisi sote hatuna Baba mmoja? Mungu aliyetuumba siye mmoja tu? Basi, mbona kila mmoja wetu anamtenda ndugu yake mambo ya hiana, tukilinajisi agano la baba zetu? 11 Yuda ametenda kwa hiana, na chukizo limetendeka katika Israeli, na katika Yerusalemu; maana Yuda ameunajisi utakatifu wa Bwana aupendao, naye amemwoa binti ya mungu mgeni. 12 Bwana atamtenga mtu atendaye hayo, yeye aliye macho, na yeye ajibuye, atamtenga na hema za Yakobo, pia atamtenga yeye amtoleaye Bwana wa majeshi dhabihu. 13 Tena mnatenda haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya Bwana kwa machozi, kwa kulia na kwa kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na kuiridhia. 14 Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu Bwana amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. 15 Hakuna mtu mmoja aliyetenda hivi, ambaye alikuwa na ufahamu kidogo. Au je! Kuna mtu mmoja atafutaye mzao mwenye kumcha Mungu? Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. 16 Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana, Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana. 17 Mmemchokesha Bwana kwa maneno yenu. Lakini ninyi mwasema, Tumemchokesha kwa maneno gani? Kwa kuwa mwasema, Kila atendaye mabaya ni mwema machoni pa Bwana, naye huwafurahia watu hao, au, Mungu mwenye kuhukumu yuko wapi?

Malaki 3

1 Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam, yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema Bwana wa majeshi. 2 Lakini ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? Au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo; 3 naye ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa, naye atawatakasa wana wa Lawi, atawasafisha kama dhahabu na fedha; nao watamtolea Bwana dhabihu katika haki. 4 Wakati ule ndipo dhabihu za Yuda na Yerusalemu zitakapopendeza mbele za Bwana, kama katika siku za kale, na kama katika miaka ya zamani. 5 Nami nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi, na juu ya wazinzi, na juu yao waapao kwa uongo; na juu yao wamwoneao mwenye kuajiriwa, kwa ajili ya mshahara wake, wamwoneao mjane na yatima, na kumpotosha mgeni asipate haki yake, wala hawaniogopi mimi, asema Bwana wa majeshi. 6 Kwa kuwa mimi, Bwana, sina kigeugeu; ndio maana ninyi hamkuangamizwa, enyi wana wa Yakobo. 7 Tokea siku za baba zenu mmegeuka upande, mkayaacha maagizo yangu, wala hamkuyashika. Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi. Lakini ninyi mwasema, Turudi kwa namna gani? 8 Je! Mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, Tumekuibia kwa namna gani? Mmeniibia zaka na dhabihu. 9 Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia mimi, naam, taifa hili lote. 10 Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema Bwana wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la. 11 Nami kwa ajili yenu nitamkemea yeye alaye, wala hataharibu mazao ya ardhi yenu; wala mzabibu wenu hautapukutisha matunda yake kabla ya wakati wake katika mashamba, asema Bwana wa majeshi. 12 Na mataifa yote watawaiteni heri; maana mtakuwa nchi ya kupendeza sana, asema Bwana wa majeshi. 13 Maneno yenu yamekuwa magumu juu yangu, asema Bwana. Lakini ninyi mwasema, Tumesema maneno juu yako kwa namna gani? 14 Mmesema, Kumtumikia Mungu hakuna faida; na, Tumepata faida gani kwa kuyashika maagizo yake, na kwa kwenda kwa huzuni mbele za Bwana wa majeshi? 15 Na sasa twasema ya kwamba wenye kiburi ndio walio heri; naam, watendao uovu ndio wajengwao; naam, wamjaribuo Mungu ndio waponywao. 16 Ndipo wale waliomcha Bwana waliposemezana wao kwa wao. Naye Bwana akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha Bwana, na kulitafakari jina lake. 17 Nao watakuwa wangu, asema Bwana wa majeshi, katika siku ile niifanyayo; naam, watakuwa hazina yangu hasa; nami nitawaachilia, kama vile mtu amwachiliavyo mwanawe mwenyewe amtumikiaye. 18 Ndipo mtakaporudi, nanyi mtapambanua kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.

Malaki 4

1 Kwa maana, angalieni, siku ile inakuja, inawaka kama tanuru; na watu wote wenye kiburi, nao wote watendao uovu, watakuwa makapi; na siku ile inayokuja itawateketeza, asema Bwana wa majeshi; hata haitawaachia shina wala tawi. 2 Lakini kwenu ninyi mnaolicha jina langu, jua la haki litawazukia, lenye kuponya katika mbawa zake; nanyi mtatoka nje, na kucheza-cheza kama ndama wa mazizini. 3 Nanyi mtawakanyaga waovu; maana watakuwa majivu chini ya nyayo za miguu yenu; katika siku ile niifanyayo, asema Bwana wa majeshi. 4 Ikumbukeni torati ya Musa, mtumishi wangu, niliyomwamuru huko Horebu kwa ajili ya Israeli wote, naam, amri na hukumu. 5 Angalieni, nitawapelekea Eliya nabii, kabla haijaja siku ile ya Bwana, iliyo kuu na kuogofya. 6 Naye ataigeuza mioyo ya baba iwaelekee watoto wao, na mioyo ya watoto iwaelekee baba zao, ili nisije nikaipiga dunia kwa laana.

The New Testament of our Lord and Saviour Jesus Christ

Mathayo 1

1 Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. 2 Ibrahimu alimzaa Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake; 3 Yuda akamzaa Peresi na Zera kwa Tamari; Peresi akamzaa Esromu; Esromu akamzaa Aramu; 4 Aramu akamzaa Aminadabu; Aminadabu akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; 5 Salmoni akamzaa Boazi kwa Rahabu; Boazi akamzaa Obedi kwa Ruthu; Obedi akamzaa Yese; 6 Yese akamzaa mfalme Daudi. 7 Sulemani akamzaa Rehoboamu; Rehoboamu akamzaa Abiya; Abiya akamzaa Asa; 8 Asa akamzaa Yehoshafati; Yehoshafati akamzaa Yoramu; Yoramu akamzaa Uzia; 9 Uzia akamzaa Yothamu; Yothamu akamzaa Ahazi; Ahazi akamzaa Hezekia; 10 Hezekia akamzaa Manase; Manase akamzaa Amoni; Amoni akamzaa Yosia; 11 Yosia akamzaa Yekonia na ndugu zake, wakati wa ule uhamisho wa Babeli. 12 Na baada ya ule uhamisho wa Babeli, Yekonia akamzaa Shealtieli; Shealtieli akamzaa Zerubabeli; 13 Zerubabeli akamzaa Abihudi; Abihudi akamzaa Eliakimu; Eliakimu akamzaa Azori; 14 Azori akamzaa Sadoki; Sadoki akamzaa Akimu; Akimu akamzaa Eliudi; 15 Eliudi akamzaa Eleazari; Eleazari akamzaa Matani; Matani akamzaa Yakobo; 16 Yakobo akamzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa YESU aitwaye Kristo. 17 Basi vizazi vyote tangu Ibrahimu hata Daudi ni vizazi kumi na vinne; na tangu Daudi hata ule uhamisho wa Babeli ni vizazi kumi na vinne; na tangu ule uhamisho wa Babeli hata Kristo ni vizazi kumi na vinne. 18 Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. 19 Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri. 20 Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. 21 Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. 22 Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, 23 Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi. 24 Naye Yusufu alipoamka katika usingizi, alifanya kama malaika wa Bwana alivyomwagiza; akamchukua mkewe; 25 asimjue kamwe hata alipomzaa mwanawe; akamwita jina lake YESU.

Mathayo 2

1 Yesu alipozaliwa katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, tazama, mamajusi wa mashariki walifika Yerusalemu, wakisema, 2 Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tuliiona nyota yake mashariki, nasi tumekuja kumsujudia. 3 Basi mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. 4 Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao, Kristo azaliwa wapi? 5 Nao wakamwambia, Katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii, 6 Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe katika majumbe wa Yuda; Kwa kuwa kwako atatoka mtawala Atakayewachunga watu wangu Israeli. 7 Kisha Herode akawaita wale mamajusi faraghani, akapata kwao hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota. 8 Akawapeleka Bethlehemu, akasema, Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie. 9 Nao waliposikia maneno ya mfalme, walishika njia; na tazama, ile nyota waliyoiona mashariki ikawatangulia, hata ikaenda ikasimama juu ya mahali alipokuwapo mtoto. 10 Nao walipoiona ile nyota, walifurahi furaha kubwa mno. 11 Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na manemane. 12 Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine. 13 Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. 14 Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri; 15 akakaa huko hata alipokufa Herode; ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii, akisema, Kutoka Misri nalimwita mwanangu. 16 Ndipo Herode, alipoona ya kuwa amedhihakiwa na wale mamajusi, alighadhabika sana, akatuma watu akawaua watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehemu na viungani mwake mwote, tangu wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale mamajusi. 17 Ndipo lilipotimia neno lililonenwa na nabii Yeremia, akisema, 18 Sauti ilisikiwa Rama, Kilio, na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake, Asikubali kufarijiwa, kwa kuwa hawako. 19 Hata alipofariki Herode, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri, 20 akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto. 21 Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye, akafika nchi ya Israeli. 22 Lakini aliposikia ya kwamba Arkelao anamiliki huko Uyahudi mahali pa Herode babaye, aliogopa kwenda huko; naye akiisha kuonywa katika ndoto, akasafiri pande za Galilaya, 23 akaenda, akakaa katika mji ulioitwa Nazareti; ili litimie neno lililonenwa na manabii, Ataitwa Mnazorayo.

Mathayo 3

1 Siku zile aliondokea Yohana Mbatizaji akihubiri katika nyika ya Uyahudi, na kusema, 2 Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia. 3 Kwa sababu huyo ndiye aliyenenwa na nabii Isaya, akisema, Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake. 4 Naye Yohana mwenyewe alikuwa na vazi lake la singa za ngamia, na mshipi wa ngozi kiunoni mwake; na chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwitu. 5 Ndipo walipomwendea Yerusalemu, na Uyahudi wote, na nchi zote za kandokando ya Yordani; 6 naye akawabatiza katika mto wa Yordani, huku wakiziungama dhambi zao. 7 Hata alipoona wengi miongoni mwa Mafarisayo na Masadukayo wakiujia ubatizo wake, aliwaambia, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? 8 Basi zaeni matunda yapasayo toba; 9 wala msiwaze mioyoni mwenu kwamba, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba Mungu aweza katika mawe haya kumwinulia Ibrahimu watoto. 10 Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni. 11 Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto. 12 Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake; na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika. 13 Wakati huo Yesu akaja kutoka Galilaya mpaka Yordani kwa Yohana ili abatizwe. 14 Lakini Yohana alitaka kumzuia, akisema, Mimi nahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu? 15 Yesu akajibu akamwambia, Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote. Basi akamkubali. 16 Naye Yesu alipokwisha kubatizwa mara akapanda kutoka majini; na tazama, mbingu zikamfunukia, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua, akija juu yake; 17 na tazama, sauti kutoka mbinguni ikisema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.

Mathayo 4

1 Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi. 2 Akafunga siku arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa. 3 Mjaribu akamjia akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe mikate. 4 Naye akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu. 5 Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, 6 akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe. 7 Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako. 8 Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, 9 akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia. 10 Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. 11 Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia. 12 Basi Yesu aliposikia ya kwamba Yohana amefungwa, alikwenda zake mpaka Galilaya; 13 akatoka Nazareti, akaja akakaa Kapernaumu, mji ulioko pwani, mipakani mwa Zabuloni na Naftali; 14 ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, 15 Nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali, Njia ya bahari, ng'ambo ya Yordani, Galilaya ya mataifa, 16 Watu wale waliokaa katika giza Wameona mwanga mkuu, Nao waliokaa katika nchi na uvuli wa mauti Mwanga umewazukia. 17 Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia. 18 Naye alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya, aliona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea nduguye, wakitupa jarife baharini; kwa maana walikuwa wavuvi. 19 Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu. 20 Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. 21 Akaendelea mbele, akaona ndugu wengine wawili, Yakobo wa Zebedayo, na Yohana nduguye, ambao walikuwamo chomboni pamoja na Zebedayo baba yao, wakizitengeneza nyavu zao; akawaita. 22 Mara wakakiacha chombo na baba yao, wakamfuata. 23 Naye alikuwa akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri Habari Njema ya ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu. 24 Na habari zake zikaenea katika Shamu yote; wakamletea wote waliokuwa hawawezi, walioshikwa na maradhi mbalimbali na mateso, wenye pepo, na wenye kifafa, na wenye kupooza; akawaponya. 25 Na makutano mengi wakamfuata, kutoka Galilaya, na Dekapoli, na Yerusalemu, na Uyahudi, na ng'ambo ya Yordani

Mathayo 5

1 Naye alipowaona makutano, alipanda mlimani; na alipokwisha kuketi, wanafunzi wake walimjia; 2 akafumbua kinywa chake, akawafundisha, akisema, 3 Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao. 4 Heri wenye huzuni; Maana hao watafarijika. 5 Heri wenye upole; Maana hao watairithi nchi. 6 Heri wenye njaa na kiu ya haki; Maana hao watashibishwa. 7 Heri wenye rehema; Maana hao watapata rehema. 8 Heri wenye moyo safi; Maana hao watamwona Mungu. 9 Heri wapatanishi; Maana hao wataitwa wana wa Mungu. 10 Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki; Maana ufalme wa mbinguni ni wao. 11 Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. 12 Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu. 13 Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. 14 Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. 15 Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. 16 Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni. 17 Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. 18 Kwa maana, amin, nawaambia,Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka,yodi moja wala nukta moja ya torati haitaoondoka,hata yote yatimie. 19 Basi mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. 20 Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. 21 Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue, na mtu akiua, itampasa hukumu. 22 Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto. 23 Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, 24 iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. 25 Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. 26 Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho. 27 Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; 28 lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake. 29 Jicho lako la kuume likikukosesha, ling'oe ulitupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum. 30 Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum. 31 Imenenwa pia, Mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka; 32 lakini mimi nawaambia, Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini. 33 Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiape uongo, ila mtimizie Bwana nyapo zako; 34 lakini mimi nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; 35 wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu. 36 Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. 37 Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu. 38 Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; 39 Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. 40 Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. 41 Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili. 42 Akuombaye, mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo. 43 Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; 44 lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, 45 ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. 46 Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo? 47 Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo? 48 Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.

Mathayo 6

1 Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni. 2 Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu. 3 Amin, nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; 4 sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi. 5 Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao. 6 Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi. 7 Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. 8 Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba. 9 Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, 10 Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni. 11 Utupe leo riziki yetu. 12 Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. 13 Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina. 14 Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. 15 Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu. 16 Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. 17 Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; 18 ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi. 19 Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; 20 bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; 21 kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako. 22 Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. 23 Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo! 24 Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali. 25 Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? 26 Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? 27 Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? 28 Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti 29 nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. 30 Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? 31 Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? 32 Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. 33 Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. 34 Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.

Mathayo 7

1 Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi. 2 Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa. 3 Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? 4 Au utamwambiaje nduguyo, Niache nikitoe kibanzi katika jicho lako; na kumbe! Mna boriti ndani ya jicho lako mwenyewe? 5 Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako. 6 Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua. 7 Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; 8 kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. 9 Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? 10 Au akiomba samaki, atampa nyoka? 11 Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao? 12 Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii. 13 Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. 14 Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache. 15 Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali. 16 Mtawatambua kwa matunda yao. Je! Watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? 17 Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. 18 Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. 19 Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. 20 Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua. 21 Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. 22 Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? 23 Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu. 24 Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; 25 mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. 26 Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; 27 mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa. 28 Ikawa, Yesu alipoyamaliza maneno hayo, makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake; 29 kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao.

Mathayo 8

1 Naye aliposhuka mlimani, makutano mengi walimfuata. 2 Na tazama, akaja mtu mwenye ukoma akamsujudia, akisema, Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa. 3 Yesu akanyosha mkono, akamgusa, akisema Nataka; takasika. Na mara ukoma wake ukatakasika. 4 Yesu akamwambia, Angalia, usimwambie mtu; ila enenda zako, ukajionyeshe kwa kuhani, ukaitoe sadaka kama alivyoamuru Musa, iwe ushuhuda kwao. 5 Hata alipoingia Kapernaumu, akida mmoja alimjia, 6 akamsihi, akisema, Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani, mgonjwa wa kupooza, anaumwa sana. 7 Yesu akamwambia, Nitakuja, nimponye. 8 Yule akida akamjibu, akasema, Bwana, mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu; lakini sema neno tu, na mtumishi wangu atapona. 9 Kwa maana mimi nami ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, mwenye askari chini yangu; nikimwambia huyu, Nenda, huenda; na huyu, Njoo, huja; na mtumwa wangu, Fanya hivi, hufanya. 10 Yesu aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni, Sijaona imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli. 11 Nami nawaambieni, ya kwamba wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi, nao wataketi pamoja na Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo katika ufalme wa mbinguni; 12 bali wana wa ufalme watatupwa katika giza la nje, ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. 13 Naye Yesu akamwambia yule akida, Nenda zako; na iwe kwako kama ulivyoamini. Mtumishi wake akapona saa ile ile. 14 Hata Yesu alipofika nyumbani kwa Petro, akamwona mkwe wa Petro, mamaye mkewe, amelala kitandani hawezi homa. 15 Akamgusa mkono, homa ikamwacha; naye akaondoka, akawatumikia. 16 Hata kulipokuwa jioni, wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, 17 ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu. 18 Naye Yesu alipoona makutano mengi wakimzunguka, aliamuru kuvuka kwenda ng'ambo. 19 Mwandishi mmoja akamwendea, akamwambia, Mwalimu, nitakufuata ko kote uendako. 20 Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota; lakini Mwana wa Adamu hana pa kulaza kichwa chake. 21 Mwingine katika wanafunzi wake akamwambia, Bwana, nipe ruhusa kwanza, niende nikamzike baba yangu. 22 Lakini Yesu akamwambia, Nifuate; waache wafu wazike wafu wao. 23 Akapanda chomboni, wanafunzi wake wakamfuata. 24 Kukawa msukosuko mkuu baharini, hata chombo kikafunikizwa na mawimbi; naye alikuwa amelala usingizi. 25 Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia. 26 Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari; kukawa shwari kuu. 27 Wale watu wakamaka wakisema, Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii? 28 Naye alipofika ng'ambo, katika nchi ya Wagerasi, watu wawili wenye pepo walikutana naye, wanatoka makaburini, wakali mno, hata mtu asiweze kuipitia njia ile. 29 Na tazama, wakapiga kelele, wakisema, Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je! Umekuja kututesa kabla ya muhula wetu? 30 Basi, kulikuwako mbali nao kundi la nguruwe wengi wakilisha. 31 Wale pepo wakamsihi, wakisema, Ukitutoa, tuache twende, tukaingie katika lile kundi la nguruwe. 32 Akawaambia, Nendeni. Wakatoka, wakaingia katika nguruwe; na kumbe! Kundi lote wakatelemka kwa kasi gengeni hata baharini, wakafa majini. 33 Lakini wachungaji walikimbia, wakaenda zao mjini, wakazieneza habari zote na habari za wale wenye pepo pia. 34 Na tazama, mji wote ukatoka kwenda kumlaki Yesu; nao walipomwona, walimsihi aondoke mipakani mwao.

Mathayo 9

1 Akapanda chomboni, akavuka, akafika mjini kwao. 2 Na tazama, wakamletea mtu mwenye kupooza, amelala kitandani; naye Yesu, alipoiona imani yao, alimwambia yule mwenye kupooza, Jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako. 3 Na tazama, baadhi ya waandishi wakasema nafsini mwao, Huyu anakufuru. 4 Naye Yesu, hali akijua mawazo yao, akasema, Mbona mnawaza maovu mioyoni mwenu? 5 Kwa maana rahisi ni lipi, ni kusema, Umesamehewa dhambi zako, au ni kusema, Ondoka, uende? 6 Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako. 7 Akaondoka, akaenda zake nyumbani kwake. 8 Makutano walipomwona, walishikwa na hofu, wakamtukuza Mungu, aliyewapa watu amri ya namna hii. 9 Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata. 10 Ikawa alipoketi nyumbani ale chakula, tazama, watoza ushuru wengi na wenye dhambi walikuja wakaketi pamoja na Yesu na wanafunzi wake. 11 Mafarisayo walipoona, waliwaambia wanafunzi wake, Mbona mwalimu wenu anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? 12 Naye aliposikia, aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi. 13 Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi. 14 Wakati ule wanafunzi wake Yohana wakamwendea, wakasema, Kwa nini sisi na Mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi? 15 Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga. 16 Hakuna mtu atiaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; maana kile kilichotiwa huondoa kipande cha lile vazi, na pale palipotatuka huzidi. 17 Wala watu hawatii divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama wakitia, vile viriba hupasuka, divai ikamwagika, na viriba vikaharibika; bali hutia divai mpya katika viriba vipya, vikahifadhika vyote. 18 Alipokuwa akiwaambia hayo, tazama, akaja jumbe mmoja, akamsujudia, akisema, Binti yangu sasa hivi amekufa; lakini njoo, uweke mkono wako juu yake, naye ataishi. 19 Akaondoka Yesu, akamfuata, pamoja na wanafunzi wake. 20 Na tazama, mwanamke aliyekuwa na ugonjwa wa kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, alikuja kwa nyuma, akaugusa upindo wa vazi lake. 21 Kwa maana alisema moyoni mwake, Nikigusa tu upindo wa vazi lake nitapona. 22 Yesu akageuka, akamwona, akamwambia, Jipe moyo mkuu, binti yangu; imani yako imekuponya. Yule mwanamke akapona tangu saa ile. 23 Yesu alipofika nyumbani kwa yule jumbe, aliona wapiga filimbi, na makutano wakifanya maombolezo, 24 akawaambia, Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu. Wakamcheka sana. 25 Lakini makutano walipoondoshwa, aliingia, akamshika mkono; yule kijana akasimama. 26 Zikaenea habari hizi katika nchi ile yote. 27 Yesu alipokuwa akipita kutoka huko, vipofu wawili wakamfuata wakipaza sauti, wakisema, Uturehemu, Mwana wa Daudi. 28 Naye alipofika nyumbani, wale vipofu walimwendea; Yesu akawaambia, Mnaamini kwamba naweza kufanya hili? Wakamwambia, Naam, Bwana. 29 Ndipo alipowagusa macho, akasema, Kwa kadiri ya imani yenu mpate. 30 Macho yao yakafumbuka. Naye Yesu akawaagiza kwa nguvu, akisema, Angalieni hata mtu mmoja asijue. 31 Lakini wakatoka, wakaeneza habari zake katika nchi ile yote. 32 Hata hao walipokuwa wakitoka, tazama, walimletea mtu bubu mwenye pepo. 33 Na pepo alipotolewa, yule bubu alinena, makutano wakastajabu, wakasema, Haijaonekana hivi katika Israeli wakati wo wote. 34 Lakini Mafarisayo wakasema, Kwa nguvu za mkuu wa pepo atoa pepo. 35 Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. 36 Na alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. 37 Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. 38 Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.

Mathayo 10

1 Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. 2 Na majina ya hao mitume kumi na wawili ni haya; Wa kwanza Simoni aliyeitwa Petro, na Andrea nduguye; Yakobo wa Zebedayo, na Yohana nduguye; 3 Filipo, na Bartholomayo; Tomaso, na Mathayo mtoza ushuru; Yakobo wa Alfayo, na Thadayo; 4 Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye kumsaliti. 5 Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema, Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. 6 Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. 7 Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia. 8 Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure. 9 Msichukue dhahabu, wala fedha, wala mapesa mishipini mwenu; 10 wala mkoba wa safari, wala kanzu mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake. 11 Na mji wo wote au kijiji cho chote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo aliye mtu mwaminifu; mkae kwake hata mtakapotoka. 12 Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. 13 Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi. 14 Na mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au mji ule, kung'uteni mavumbi ya miguuni mwenu. 15 Amin, nawaambia, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma na Gomora kustahimili adhabu ya siku ya hukumu, kuliko mji ule. 16 Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua. 17 Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; 18 nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. 19 Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. 20 Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu. 21 Na ndugu atamsaliti nduguye ili auawe, na baba atamsaliti mwana, na wana watawainukia wazazi wao, na kuwafisha. 22 Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka. 23 Lakini watakapowafukuza katika mji huu, kimbilieni mwingine; kwa maana ni kweli nawaambia, Hamtaimaliza miji ya Israeli, hata ajapo Mwana wa Adamu. 24 Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, wala mtumwa hampiti bwana wake. 25 Yamtosha mwanafunzi kuwa kama mwalimu wake, na mtumwa kuwa kama bwana wake. Ikiwa wamemwita mwenye nyumba Beelzebuli, je! Si zaidi wale walio wa nyumbani mwake? 26 Basi, msiwaogope, kwa maana hakuna neno lililositirika, ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa, ambalo halitajulikana. 27 Niwaambialo ninyi katika giza, lisemeni katika nuru; na msikialo kwa siri, lihubirini juu ya nyumba. 28 Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum. 29 Je! Mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; 30 lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. 31 Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro wengi. 32 Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. 33 Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni. 34 Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga. 35 Kwa maana nalikuja kumfitini mtu na babaye, na binti na mamaye, na mkwe na mkwe mtu; 36 na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake. 37 Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili. 38 Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili. 39 Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona. 40 Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea yeye aliyenituma. 41 Ampokeaye nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki. 42 Na mtu awaye yote atakayemnywesha mmojawapo wa wadogo hawa ngaa kikombe cha maji ya baridi, kwa kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia, haitampotea kamwe thawabu yake.

Mathayo 11

1 Ikawa Yesu alipokwisha kuwaagiza wanafunzi wake kumi na wawili, alitoka huko kwenda kufundisha na kuhubiri katika miji yao. 2 Naye Yohana aliposikia huko gerezani matendo yake Kristo, alituma wanafunzi wake, kumwuliza, 3 Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? 4 Yesu akajibu akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana mnayoyasikia na kuyaona; 5 vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema. 6 Naye heri awaye yote asiyechukizwa nami. 7 Na hao walipokwenda zao, Yesu alianza kuwaambia makutano habari za Yohana, Mlitoka kwenda nyikani kutazama nini? Unyasi ukitikiswa na upepo? 8 Lakini mlitoka kwenda kuona nini? Mtu aliyevikwa mavazi mororo? Tazama, watu wavaao mavazi mororo wamo katika nyumba za wafalme. 9 Lakini kwa nini mlitoka? Ni kuona nabii? Naam, nawaambia, na aliye mkuu zaidi ya nabii. 10 Huyo ndiye aliyeandikiwa haya, Tazama, mimi namtuma mjumbe wangu Mbele ya uso wako, Atakayeitengeneza njia yako mbele yako. 11 Amin, nawaambieni, Hajaondokea mtu katika wazao wa wanawake aliye mkuu kuliko Yohana Mbatizaji; walakini aliye mdogo katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye. 12 Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatikana kwa nguvu, nao wenye nguvu wauteka. 13 Kwa maana manabii wote na torati walitabiri mpaka wakati wa Yohana. 14 Na ikiwa mnataka kukubali, yeye ndiye Eliya atakayekuja. 15 Mwenye masikio, na asikie. 16 Lakini nitakifananisha na nini kizazi hiki? Kimefanana na watoto wanaokaa sokoni, wanaowaita wenzao, wakisema, 17 Tuliwapigia filimbi, wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia. 18 Maana Yohana alikuja, hali wala hanywi, wakasema, Yuna pepo. 19 Mwana wa Adamu alikuja, akila na kunywa, wakasema, Mlafi huyu, na mlevi, rafiki yao watoza ushuru na wenye dhambi! Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi zake. 20 Ndipo akaanza kuikemea miji ile ambamo ndani yake ilifanyika miujiza yake iliyo mingi, kwa sababu haikutubu. 21 Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu. 22 Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi Tiro na Sidoni kustahimili adhabu zao siku ya hukumu kuliko ninyi. 23 Nawe Kapernaumu, je! Utakuzwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka kuzimu; kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwako ingalifanyika katika Sodoma, ungalikuwapo mji huo hata leo. 24 Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe. 25 Wakati ule Yesu akajibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. 26 Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. 27 Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia. 28 Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. 29 Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; 30 kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.

Mathayo 12

1 Wakati ule Yesu alipita katika mashamba siku ya sabato; wanafunzi wake wakaona njaa, wakaanza kuvunja masuke, wakala. 2 Na Mafarisayo walipoona, walimwambia, Tazama! Wanafunzi wako wanafanya neno ambalo si halali kulifanya siku ya sabato. 3 Akawaambia, Hamkusoma alivyotenda Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wenziwe? 4 jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaila mikate ile ya wonyesho, ambayo si halali kwake kuila wala kwa wale wenziwe, ila kwa makuhani peke yao? 5 Wala hamkusoma katika torati, kwamba siku ya sabato makuhani hekaluni huinajisi sabato wasipate hatia? 6 Lakini nawaambieni, kwamba hapa yupo aliye mkuu kuliko hekalu. 7 Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia. 8 Kwa maana Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato. 9 Akaondoka huko, akaingia katika sinagogi lao. 10 Na tazama, yumo mtu mwenye mkono umepooza; wakamwuliza, wakisema, Ni halali kuponya watu siku ya sabato? Wapate kumshitaki. 11 Akawaambia, Ni mtu yupi miongoni mwenu mwenye kondoo mmoja, na yule kondoo ametumbukia shimoni siku ya sabato, asiyemshika akamwopoa? 12 Je! Mtu ni bora kuliko kondoo mara ngapi? Basi ni halali kutenda mema siku ya sabato. 13 Kisha akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako; akaunyosha, ukapona, ukawa mzima kama wa pili. 14 Lakini wale Mafarisayo wakatoka wakafanya shauri juu yake jinsi ya kumwangamiza. 15 Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, 16 akawakataza wasimdhihirishe; 17 ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, 18 Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. 19 Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. 20 Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. 21 Na jina lake Mataifa watalitumainia. 22 Wakati ule akaletewa mtu mwenye pepo, kipofu, naye ni bubu; akamponya, hata yule bubu akanena na kuona. 23 Makutano wote wakashangaa, wakasema, Huyu siye mwana wa Daudi? 24 Lakini Mafarisayo waliposikia, walisema, Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo. 25 Basi Yesu akijua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme ukifitinika juu ya nafsi yake, hufanyika ukiwa; tena mji au nyumba yo yote ikifitinika juu ya nafsi yake, haitasimama. 26 Na Shetani akimtoa Shetani, amefitinika juu ya nafsi yake; basi ufalme wake utasimamaje? 27 Na mimi nikitoa pepo kwa Beelzebuli, je! Wana wenu huwatoa kwa nani? Kwa sababu hiyo hao ndio watakaowahukumu. 28 Lakini mimi nikitoa pepo kwa Roho wa Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia. 29 Ama awezaje mtu kuingia ndani ya nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuviteka vyombo vyake, asipomfunga kwanza yule mwenye nguvu? Ndipo atakapoiteka nyumba yake. 30 Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya. 31 Kwa sababu hiyo nawaambia, Kila dhambi na kila neno la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho hawatasamehewa. 32 Naye mtu ye yote atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali yeye atakayenena neno juu ya Roho Mtakatifu hatasamehewa katika ulimwengu wa sasa, wala katika ule ujao. 33 Ufanyeni mti kuwa mzuri na matunda yake kuwa mazuri; au ufanyeni mti kuwa mbaya na matunda yake mabaya, kwa maana kwa matunda yake mti hutambulikana. 34 Enyi wazao wa nyoka, mwawezaje kunena mema, mkiwa wabaya? Maana, kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake. 35 Mtu mwema katika akiba njema hutoa mema; na mtu mbaya katika akiba mbaya hutoa mabaya. 36 Basi, nawaambia, Kila neno lisilo maana, watakalolinena wanadamu, watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu. 37 Kwa kuwa kwa maneno yako utahesabiwa haki, na kwa maneno yako utahukumiwa. 38 Hapo baadhi ya waandishi na Mafarisayo wakamjibu, wakasema, Mwalimu, twataka kuona ishara kwako. 39 Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona. 40 Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku katika moyo wa nchi. 41 Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona. 42 Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani. 43 Pepo mchafu, amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika, asipate. 44 Halafu husema, Nitarudi nyumbani kwangu nilikotoka; hata akija, aiona tupu, imefagiwa, na kupambwa. 45 Mara huenda, akachukua pamoja naye pepo wengine saba walio waovu kuliko yeye mwenyewe, nao huingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza. Ndivyo itakavyokuwa kwa kizazi hiki kilicho kibaya. 46 Alipokuwa katika kusema na makutano, tazama, mama yake na ndugu zake walikuwa wakisimama nje, wataka kusema naye. 47 Mtu mmoja akamwambia, Tazama, mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kusema nawe. 48 Akajibu, akamwambia yule aliyempasha habari, Mama yangu ni nani? Na ndugu zangu ni akina nani? 49 Akawanyoshea mkono wanafunzi wake, akasema, Tazama, Mama yangu na ndugu zangu! 50 Kwa maana ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.

Mathayo 13

1 Siku ile Yesu akatoka nyumbani, akaketi kando ya bahari. 2 Wakamkusanyikia makutano mengi, hata akapanda chomboni, akaketi; na ule mkutano wote wakasimama pwani. 3 Akawaambia mambo mengi kwa mifano, akisema, Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda. 4 Hata alipokuwa akipanda, mbegu nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila; 5 nyingine zikaanguka penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa kina; 6 na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka. 7 Nyingine zikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga; 8 nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini. 9 Mwenye masikio na asikie. 10 Wakaja wanafunzi, wakamwambia, Kwa nini wasema nao kwa mifano? 11 Akajibu, akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. 12 Kwa maana ye yote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini ye yote asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa. 13 Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano; kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. 14 Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; Kutazama mtatazama, wala hamtaona. 15 Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, Na kwa masikio yao hawasikii vema, Na macho yao wameyafumba; Wasije wakaona kwa macho yao, Wakasikia kwa masikio yao, Wakaelewa kwa mioyo yao, Wakaongoka, nikawaponya. 16 Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia. 17 Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie. 18 Basi ninyi sikilizeni mfano wa mpanzi. 19 Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia. 20 Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha; 21 lakini hana mizizi ndani yake, bali hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara huchukizwa. 22 Naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai. 23 Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini. 24 Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; 25 lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake. 26 Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. 27 Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu? 28 Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye? 29 Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing'oa ngano pamoja nayo. 30 Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu. 31 Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na punje ya haradali, aliyoitwaa mtu akaipanda katika shamba lake; 32 nayo ni ndogo kuliko mbegu zote; lakini ikiisha kumea, huwa kubwa kuliko mboga zote, ikawa mti, hata nyuni wa angani huja na kukaa katika matawi yake. 33 Akawaambia mfano mwingine; Ufalme wa mbinguni umefanana na chachu aliyoitwaa mwanamke, akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachachwa wote pia. 34 Hayo yote Yesu aliwaambia makutano kwa mifano; wala pasipo mfano hakuwaambia neno; 35 ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Nitafumbua kinywa changu kwa mifano, Nitayatamka yaliyositirika tangu awali. 36 Kisha Yesu akawaaga makutano, akaingia nyumbani; wanafunzi wake wakamwendea, wakasema, Tufafanulie mfano wa magugu ya kondeni. 37 Akajibu, akasema, Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu; 38 lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu; 39 yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wavunao ni malaika. 40 Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia. 41 Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote, na hao watendao maasi, 42 na kuwatupa katika tanuru ya moto, ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. 43 Ndipo wenye haki watakapong'aa kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio, na asikie. 44 Tena ufalme wa mbinguni umefanana na hazina iliyositirika katika shamba; ambayo mtu alipoiona, aliificha; na kwa furaha yake akaenda akauza alivyo navyo vyote, akalinunua shamba lile. 45 Tena ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri; 46 naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akainunua. 47 Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna; 48 hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa. 49 Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, 50 na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. 51 Yesu aliwauliza, Mmeyafahamu hayo yote? Wakamwambia, Naam. 52 Akawaambia, Kwa sababu hiyo, kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni amefanana na mtu mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale. 53 Ikawa Yesu alipoimaliza mifano hiyo, alitoka akaenda zake. 54 Na alipofika nchi yake, akawafundisha katika sinagogi lao, hata wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii? 55 Huyu si mwana wa seremala? Mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, na Yusufu, na Simoni, na Yuda? 56 Na maumbu yake wote hawapo hapa petu? Basi huyu amepata wapi haya yote? 57 Wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe. 58 Wala hakufanya miujiza mingi huko, kwa sababu ya kutokuamini kwao.

Mathayo 14

1 Wakati ule mfalme Herode alisikia habari za Yesu, akawaambia watumishi wake, 2 Huyo ndiye Yohana Mbatizaji; amefufuka katika wafu; na kwa hiyo nguvu hizo zinatenda kazi ndani yake. 3 Maana Herode alikuwa amemkamata Yohana, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye. 4 Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye. 5 Naye alipotaka kumwua, aliwaogopa watu, maana walimwona Yohana kuwa nabii. 6 Hata ilipofika sikukuu ya kuzaliwa kwake Herode, binti Herodia alicheza mbele ya watu, akampendeza Herode. 7 Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba. 8 Naye, huku akichochewa na mamaye, akasema, Nipe hapa katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji. 9 Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; 10 akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani. 11 Kichwa chake kikaletwa katika kombe, akapewa yule kijana; akakichukua kwa mamaye. 12 Wanafunzi wake wakaenda, wakamchukua yule maiti, wakamzika; kisha wakaenda wakampasha Yesu habari. 13 Naye Yesu aliposikia; hayo, aliondoka huko katika chombo, akaenda mahali pasipo watu, faraghani. Na makutano waliposikia, walimfuata kwa miguu kutoka mijini mwao. 14 Yesu akatoka, akaona mkutano mkuu, akawahurumia, akawaponya wagonjwa wao. 15 Hata kulipokuwa jioni, wanafunzi wake walimwendea, wakasema, Mahali hapa ni nyika tupu, na saa imekwisha pita; uwaage makutano, waende zao vijijini, wakajinunulie vyakula. 16 Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula. 17 Wakamwambia, Hamna kitu hapa ila mikate mitano na samaki wawili. 18 Akasema, Nileteeni hapa. 19 Akawaagiza makutano waketi katika majani; akaitwaa ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama juu mbinguni, akabariki, akaimega ile mikate, akawapa wanafunzi, wanafunzi wakawapa makutano. 20 Wakala wote wakashiba; wakayaokota masazo ya vipande vya mikate, vikapu kumi na viwili, vimejaa. 21 Nao waliokula walikuwa wanaume wapata elfu tano, bila wanawake na watoto. 22 Mara akawalazimisha wanafunzi wake wapande chomboni na kutangulia mbele yake kwenda ng'ambo, wakati yeye alipokuwa akiwaaga mkutano. 23 Naye alipokwisha kuwaaga makutano, alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake. 24 Na kile chombo kimekwisha kufika katikati ya bahari, kinataabika sana na mawimbi; maana upepo ulikuwa wa mbisho. 25 Hata wakati wa zamu ya nne ya usiku Yesu akawaendea, akienda kwa miguu juu ya bahari. 26 Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli; wakapiga yowe kwa hofu. 27 Mara Yesu alinena, akawaambia, Jipeni moyo ni mimi; msiogope. 28 Petro akamjibu, akasema, Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji. 29 Akasema, Njoo. Petro akashuka chomboni, akaenda kwa miguu juu ya maji, ili kumwendea Yesu. 30 Lakini alipouona upepo, akaogopa; akaanza kuzama, akapiga yowe, akisema, Bwana, niokoe. 31 Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka? 32 Nao walipopanda chomboni, upepo ulikoma. 33 Nao waliokuwamo ndani ya chombo wakamsujudia, wakisema, Hakika wewe u Mwana wa Mungu. 34 Na walipokwisha kuvuka, walifika nchi ya Genesareti. 35 Na watu wa mahali pale walipomtambua, walituma watu kwenda nchi zile zilizo kandokando, wakamletea wote waliokuwa hawawezi; 36 nao wakamsihi waguse hata pindo la vazi lake tu; na wote waliogusa wakaponywa kabisa.

Mathayo 15

1 Ndipo Mafarisayo na waandishi toka Yerusalemu walipomwendea Yesu wakisema, 2 Mbona wanafunzi wako huyahalifu mapokeo ya wazee, kwa maana hawanawi mikono walapo chakula. 3 Akajibu, akawaambia, Mbona ninyi nanyi huihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu? 4 Kwa kuwa Mungu alisema, Mheshimu baba yako na mama yako, na Amtukanaye baba yake au mama yake kufa na afe. 5 Bali ninyi husema, Atakayemwambia babaye au mamaye, Cho chote kikupasacho kusaidiwa na mimi ni wakfu, 6 basi asimheshimu baba yake au mama yake. Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu. 7 Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, 8 Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami. 9 Nao waniabudu bure, Wakifundisha mafundisho Yaliyo maagizo ya wanadamu. 10 Akawaita makutano akawaambia 11 Sikilizeni, mfahamu; Sicho kiingiacho kinywani kimtiacho mtu unajisi; bali kitokacho kinywani ndicho kimtiacho mtu unajisi. 12 Ndipo wanafunzi wake walipomwendea, wakamwambia, Wajua ya kuwa Mafarisayo walipolisikia neno lile walichukizwa? 13 Akajibu, akasema, Kila pando asilolipanda Baba yangu wa mbinguni litang'olewa. 14 Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili. 15 Basi Petro akajibu, akamwambia, Tueleze mfano huo. 16 Yesu akasema, Hata sasa ninyi nanyi mngali hamna akili? 17 Hamjafahamu bado ya kuwa kila kiingiacho kinywani hupita tumboni, kikatupwa chooni? 18 Bali vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi. 19 Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati; wivi, ushuhuda wa uongo, na matukano; 20 hayo ndiyo yamtiayo mtu unajisi; lakini kula kabla hajanawa mikono hakumtii mtu unajisi. 21 Yesu akaondoka huko, akaenda kando pande za Tiro na Sidoni. 22 Na tazama, mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, Mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo. 23 Wala yeye hakumjibu neno. Nao wanafunzi wake wakamwendea, wakamwomba, wakisema, Mwache aende zake; kwa maana anapiga kelele nyuma yetu. 24 Akajibu, akasema, Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. 25 Naye akaja akamsujudia, akisema Bwana, unisaidie. 26 Akajibu, akasema, Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. 27 Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. 28 Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, Mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile. 29 Yesu akaondoka huko, akafika kando ya bahari ya Galilaya; akapanda mlimani, akaketi huko. 30 Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya; 31 hata ule mkutano wakastaajabu, walipowaona mabubu wanasema, vilema wanakuwa wazima, viwete wanakwenda, na vipofu wanaona; wakamtukuza Mungu wa Israeli. 32 Yesu akawaita wanafunzi wake, akasema, Nawahurumia mkutano, kwa kuwa yapata siku tatu wamekaa pamoja nami, wala hawana kitu cha kula, tena kuwaaga wakifunga sipendi, wasije wakazimia njiani. 33 Wanafunzi wake wakamwambia, Tupate wapi mikate mingi hapa nyikani, hata kushibisha mkutano mkuu namna hii? 34 Yesu akawaambia, Mnayo mikate mingapi? Wakasema, Saba, na visamaki vichache. 35 Akawaagiza mkutano waketi chini; 36 akaitwaa ile mikate saba na vile visamaki, akashukuru akavimega, akawapa wanafunzi wake, nao wanafunzi wakawapa makutano. 37 Wakala wote wakashiba; wakayaokota masazo ya vipande vya mikate makanda saba, yamejaa. 38 Nao waliokula walikuwa wanaume elfu nne, bila wanawake na watoto. 39 Akawaaga makutano, akapanda chomboni, akaenda pande za Magadani.

Mathayo 16

1 Wakamjia Mafarisayo na Masadukayo, wakamjaribu, wakamwomba awaonyeshe ishara itokayo mbinguni. 2 Akajibu, akawaambia, Kukiwa jioni, mwasema, Kutakuwa na kianga; kwa maana mbingu ni nyekundu. 3 Na asubuhi, mwasema, Leo kutakuwa na dhoruba; kwa maana mbingu ni nyekundu, tena kumetanda. Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa mbingu; lakini, je! Ishara za zamani hizi hamwezi kuzitambua? 4 Kizazi kibaya na cha zinaa chataka ishara; wala hakitapewa ishara, isipokuwa ishara ya Yona. Akawaacha, akaenda zake. 5 Nao wanafunzi wakaenda hata ng'ambo, wakasahau kuchukua mikate. 6 Yesu akawaambia, Angalieni, jilindeni na chachu ya Mafarisayo na Masadukayo. 7 Wakabishana wao kwa wao, wakisema, Ni kwa sababu hatukuchukua mikate. 8 Naye Yesu akafahamu, akawaambia, Mbona mnabishana ninyi kwa ninyi, enyi wa imani chache, kwa sababu hamna mikate? 9 Hamjafahamu bado, wala hamkumbuki ile mikate mitano kwa wale elfu tano, na vikapu vingapi mlivyoviokota? 10 Wala ile mikate saba kwa watu elfu nne, na makanda mangapi mliyoyaokota? 11 Imekuwaje hamkufahamu ya kuwa si kwa sababu ya mkate naliwaambia? Ila jilindeni na chachu ya Mafarisayo na Masadukayo. 12 Ndipo walipofahamu ya kuwa hakuwaambia kujilinda na chachu ya mkate, bali na mafundisho ya Mafarisayo na Masadukayo. 13 Basi Yesu akaenda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa ni nani? 14 Wakasema, Wengine hunena u Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii. 15 Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani? 16 Simoni Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. 17 Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. 18 Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda. 19 Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni. 20 Ndipo alipowakataza sana wanafunzi wake wasimwambie mtu ye yote ya kwamba yeye ndiye Kristo. 21 Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. 22 Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema, Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. 23 Akageuka, akamwambia Petro, Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu. 24 Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate. 25 Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona. 26 Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake? 27 Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake. 28 Amin, nawaambieni, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika ufalme wake.

Mathayo 17

1 Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; 2 akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. 3 Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. 4 Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. 5 Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye. 6 Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana. 7 Yesu akaja, akawagusa, akasema, Inukeni, wala msiogope. 8 Wakainua macho yao, wasione mtu ila Yesu peke yake. 9 Na walipokuwa wakishuka mlimani, Yesu aliwaagiza, akasema, Msimwambie mtu ye yote habari ya maono hayo, hata Mwana wa Adamu atakapofufuka katika wafu. 10 Wanafunzi wake wakamwuliza, wakisema, Basi kwa nini waandishi hunena ya kwamba imempasa Eliya kuja kwanza? 11 Naye akajibu, akawaambia, Kweli Eliya yuaja kwanza, naye atatengeneza yote, 12 ila nawaambia, ya kwamba Eliya amekwisha kuja, wasimtambue, lakini wakamtenda yote waliyotaka. Vivyo hivyo Mwana wa Adamu naye yuaenda kuteswa kwao. 13 Ndipo wale wanafunzi walipofahamu ya kuwa amesema nao habari za Yohana Mbatizaji. 14 Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, akampigia magoti, akisema, 15 Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. 16 Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. 17 Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. 18 Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. 19 Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? 20 Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. 21 Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga. 22 Nao walipokuwa wakikaa Galilaya, Yesu akawaambia, Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua, na siku ya tatu atafufuka. 23 Wakasikitika sana. 24 Hata walipofika Kapernaumu, wale watozao nusu-shekeli walimwendea Petro, wakasema, Je! Mwalimu wenu hatoi nusu-shekeli? Akasema, Hutoa. 25 Naye alipoingia nyumbani, Yesu alitangulia kumwuliza, akisema, Waonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hutwaa kodi ama ushuru kwa watu gani? Kwa wana wao au kwa wageni? 26 Naye aliposema, Kwa wageni, Yesu alimwambia, Basi, kama ni hivyo, wana ni mahuru. 27 Lakini tusije tukawakwaza, enenda baharini ukatupe ndoana, ukatwae samaki yule azukaye kwanza; na ukifumbua mdomo wake utaona shekeli ichukue hiyo ukawape kwa ajili yangu na kwa ajili yako.

Mathayo 18

1 Saa ile wanafunzi wakamwendea Yesu wakisema, 2 Ni nani basi aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni? Akaita mtoto mmoja, akamweka katikati yao, 3 akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. 4 Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni. 5 Na ye yote atakayempokea mtoto mmoja mfano wa huyu kwa jina langu, anipokea mimi; 6 bali atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari. 7 Ole ni wa ulimwengu kwa sababu ya mambo ya kukosesha! Maana hayana budi kuja mambo ya kukosesha; lakini ole wake mtu yule aliletaye jambo la kukosesha! 8 Basi mkono wako au mguu wako ukikukosesha, ukate ukautupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima hali umepungukiwa na mkono au mguu, kuliko kuwa na mikono miwili au miguu miwili, na kutupwa katika moto wa milele. 9 Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ukalitupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum ya moto. 10 Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni. 11 Kwa maana Mwana wa Adamu alikuja kukiokoa kilichopotea. 12 Mwaonaje? Mtu akiwa na kondoo mia, mmoja akampotea, je! Hawaachi wale tisa na tisini, akaenda milimani, na kumtafuta yule aliyepotea? 13 Hata akipata kumwona, amin, nawaambia, amfurahia huyo zaidi, kuliko wale tisa na tisini wasiopotea. 14 Vivyo hivyo haipendezi mbele za Baba yenu aliye mbinguni kwamba mmoja wa wadogo hawa apotee. 15 Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. 16 La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. 17 Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru. 18 Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. 19 Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. 20 Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao. 21 Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? 22 Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini. 23 Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. 24 Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. 25 Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni. 26 Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. 27 Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. 28 Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia akamkamata,akamshika koo,akisema Nilipe uwiwacho. 29 Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. 30 Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa ile deni. 31 Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. 32 Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi; 33 nawe, je! Haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? 34 Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. 35 Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.

Mathayo 19

1 Ikawa Yesu alipomaliza maneno hayo, akatoka Galilaya akafika mipaka ya Uyahudi, ng'ambo ya Yordani. 2 Makutano mengi wakamfuata, akawaponya huko. 3 Basi Mafarisayo wakamwendea, wakamjaribu, wakimwambia, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe kwa kila sababu? 4 Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, 5 akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? 6 Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe. 7 Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha? 8 Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. 9 Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini. 10 Wanafunzi wake wakamwambia, Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa. 11 Lakini yeye akawaambia, Si wote wawezao kulipokea neno hili, ila wale waliojaliwa. 12 Maana wako matowashi waliozaliwa hali hiyo toka matumboni mwa mama zao; tena wako matowashi waliofanywa na watu kuwa matowashi; tena wako matowashi waliojifanya kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni. Awezaye kulipokea neno hili, na alipokee. 13 Ndipo akaletewa watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. 14 Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. 15 Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko. 16 Na tazama, mtu mmoja akamwendea akamwambia, Mwalimu, nitende jambo gani jema, ili nipate uzima wa milele? 17 Akamwambia Kwani kuniuliza habari ya wema? Aliye mwema ni mmoja. Lakini ukitaka kuingia katika uzima, zishike amri. 18 Akamwambia, Zipi? Yesu akasema, Ni hizi, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, 19 Waheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama nafsi yako. 20 Yule kijana akamwambia, Haya yote nimeyashika; nimepungukiwa na nini tena? 21 Yesu akamwambia, Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate. 22 Yule kijana alipolisikia neno lile, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi. 23 Yesu akawaambia wanafunzi wake, Amin, nawaambieni, ya kwamba itakuwa shida tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni. 24 Nawaambia tena, Ni rahisi zaidi ngamia kupenya tundu ya sindano, kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu. 25 Wanafunzi waliposikia, walishangaa mno, wakisema, Ni nani basi awezaye kuokoka? 26 Yesu akawakazia macho, akawaambia, Kwa wanadamu hilo haliwezekani; bali kwa Mungu yote yawezekana. 27 Ndipo Petro akajibu, akamwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata; tutapata nini basi? 28 Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli. 29 Na kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele. 30 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na walio wa mwisho watakuwa wa kwanza.

Mathayo 20

1 Kwa maana ufalme wa mbinguni umefanana na mtu mwenye nyumba aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu. 2 Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu. 3 Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi; 4 na hao nao akawaambia, Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa. Wakaenda. 5 Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile. 6 Hata kama saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wamesimama, akawaambia, Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi? 7 Wakamwambia, Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri. Akawaambia, enendeni nanyi katika shamba la mizabibu. 8 Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia msimamizi wake, Waite wakulima, uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza. 9 Na walipokuja wale wa saa kumi na moja, walipokea kila mtu dinari. 10 Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari. 11 Basi wakiisha kuipokea, wakamnung'unikia mwenye nyumba, 12 wakisema, Hao wa mwisho wametenda kazi saa moja tu, nawe umewasawazisha na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa. 13 Naye akamjibu mmoja wao, akamwambia, Rafiki, sikudhulumu; hukupatana nami kwa dinari? 14 Chukua iliyo yako, uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. 15 Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema? 16 Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho. 17 Hata Yesu alipokuwa akipanda kwenda Yerusalemu, aliwachukua wale wanafunzi kumi na wawili faraghani; na njiani akawaambia, 18 Angalieni, tunapanda kwenda Yerusalemu; na Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi; nao watamhukumu afe; 19 kisha watampeleka kwa Mataifa wapate kumdhihaki, na kumpiga mijeledi, na kumsulibisha; na siku ya tatu atafufuka. 20 Ndipo mama yao wana wa Zebedayo akamwendea pamoja na wanawe, akamsujudia, na kumwomba neno. 21 Akamwambia, Wataka nini? Akamwambia, Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako. 22 Yesu akajibu akasema, Hamjui mnaloliomba. Je! Mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi? Wakamwambia, Twaweza. 23 Akawaambia, Hakika mtakinywea kikombe changu; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu. 24 Na wale kumi waliposikia, waliwakasirikia wale ndugu wawili. 25 Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. 26 Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; 27 na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; 28 kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi. 29 Hata walipokuwa wakitoka Yeriko mkutano mkubwa wakamfuata. 30 Na tazama, vipofu wawili wameketi kando ya njia, nao waliposikia ya kwamba Yesu anapita, walipaza sauti, wakisema, Uturehemu, Bwana, mwana wa Daudi! 31 Mkutano wakawakaripia, wanyamaze. Lakini wao wakazidi kupaza sauti, wakisema, Uturehemu, Bwana, mwana wa Daudi! 32 Yesu akasimama, akawaita, akasema, Mnataka niwafanyie nini? 33 Wakamwambia, Bwana, twataka macho yetu yafumbuliwe. 34 Yesu akawahurumia, akawagusa macho yao; mara wakapata kuona, wakamfuata.

Mathayo 21

1 Hata walipokaribia Yerusalemu, na kufika Bethfage, katika mlima wa Mizeituni, ndipo Yesu alipotuma wanafunzi wawili akiwaambia, 2 Enendeni mpaka kijiji kile kinachowakabili, na mara mtaona punda amefungwa, na mwana-punda pamoja naye; wafungueni mniletee. 3 Na kama mtu akiwaambia neno, semeni, Bwana anawahitaji; na mara huyo atawapeleka. 4 Haya yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, 5 Mwambieni binti Sayuni Tazama, mfalme wako anakuja kwako, Mpole, naye amepanda punda, Na mwana-punda, mtoto wa punda. 6 Wale wanafunzi wakaenda zao, wakafanya kama Yesu alivyowaamuru, 7 wakamleta yule punda na mwana-punda, wakaweka nguo zao juu yao, naye akaketi juu yake. 8 Watu wengi katika ule mkutano wakatandaza nguo zao njiani; na wengine wakakata matawi ya miti, wakayatandaza njiani. 9 Na makutano waliotangulia, na wale waliofuata, wakapaza sauti, wakisema, Hosana, Mwana wa Daudi; ndiye mbarikiwa, yeye ajaye kwa jina la Bwana; Hosana juu mbinguni. 10 Hata alipoingia Yerusalemu, mji wote ukataharuki, watu wakisema, Ni nani huyu? 11 Makutano wakasema, Huyu ni yule nabii, Yesu, wa Nazareti ya Galilaya. 12 Yesu akaingia ndani ya hekalu, akawafukuza wote waliokuwa wakiuza na kununua hekaluni, akazipindua meza za wabadili fedha, na viti vyao waliokuwa wakiuza njiwa; 13 akawaambia, Imeandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala; bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi. 14 Na vipofu na viwete wakamwendea mle hekaluni, akawaponya. 15 Lakini wakuu wa makuhani na waandishi walipoyaona maajabu aliyoyafanya, na watoto waliopaza sauti zao hekaluni, wakisema, Hosana, Mwana wa Daudi! Walikasirika, 16 wakamwambia, Wasikia hawa wasemavyo? Yesu akawaambia, Naam; hamkupata kusoma, Kwa vinywa vya watoto wachanga na wanyonyao umekamilisha sifa? 17 Akawaacha, akatoka nje ya mji mpaka Bethania, akalala huko. 18 Hata asubuhi alipokuwa akienda mjini, aliona njaa. 19 Akaona mtini mmoja kando ya njia, akauendea, asione kitu juu yake ila majani tu; akauambia, Yasipatikane matunda kwako tangu leo hata milele. Mtini ukanyauka mara. 20 Wanafunzi walipoona, walistaajabu, wakisema, Jinsi gani mtini umenyauka mara? 21 Yesu akajibu, akawaambia, Amin, nawaambia Mkiwa na imani, msipokuwa na shaka, mtafanya si hilo la mtini tu, lakini hata mkiuambia mlima huu, Ng'oka, ukatupwe baharini, litatendeka. 22 Na yo yote mtakayoyaomba katika sala mkiamini, mtapokea. 23 Hata alipokwisha kuingia hekaluni, wakuu wa makuhani na wazee wa watu wakamwendea alipokuwa akifundisha, wakasema, Ni kwa amri gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa amri hii? 24 Yesu akajibu akawaambia, Na mimi nitawauliza neno moja; ambalo mkinijibu, nami nitawaambia ni kwa amri gani ninatenda haya. 25 Ubatizo wa Yohana ulitoka wapi? Ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu? Wakahojiana wao kwa wao, wakisema, Tukisema, Ulitoka mbinguni, atatuambia, Mbona basi hamkumwamini? 26 Na tukisema, Ulitoka kwa wanadamu, twaogopa mkutano; maana watu wote wamwona Yohana kuwa ni nabii. 27 Wakamjibu Yesu wakasema, Hatujui. Naye akawaambia, Wala mimi siwaambii ninyi ni kwa amri gani ninatenda haya. 28 Lakini mwaonaje? Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo nenda kafanye kazi katika shamba la mizabibu. 29 Akajibu akasema, Naenda, Bwana; asiende. 30 Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema, Sitaki; baadaye akatubu, akaenda. 31 Je! Katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin nawaambia, watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika ufalme wa Mungu. 32 Kwa sababu Yohana alikuja kwenu kwa njia ya haki, ninyi msimwamini; lakini watoza ushuru na makahaba walimwamini, nanyi hata mlipoona, hamkutubu baadaye, ili kumwamini. 33 Sikilizeni mfano mwingine. Kulikuwa na mtu mwenye nyumba, naye alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha ugo, akachimba shimo la shinikizo ndani yake, akajenga mnara, akapangisha wakulima, akasafiri. 34 Wakati wa matunda ulipokuwa karibu, akawatuma watumwa wake kwa wale wakulima, wapokee matunda yake. 35 Wale wakulima wakawakamata watumwa wake, huyu wakampiga, na huyu wakamwua, na huyu wakampiga kwa mawe. 36 Akawatuma tena watumwa wengine wengi kuliko wa kwanza wakawatenda vile vile. 37 Mwishowe akamtuma mwanawe kwao, akisema, Watamstahi mwanangu. 38 Lakini wale wakulima walipomwona yule mwana, wakasemezana wao kwa wao, Huyu ni mrithi; haya na tumwue, tuutwae urithi wake. 39 Wakamkamata, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu, wakamwua. 40 Basi atakapokuja yule bwana wa shamba la mizabibu, atawatendaje wale wakulima? 41 Wakamwambia, Atawaangamiza vibaya wale wabaya; na shamba la mizabibu atawapangisha wakulima wengine, watakaomlipa matunda kwa wakati wake. 42 Yesu akawaambia, Hamkupata kusoma katika maandiko, Jiwe walilolikataa waashi, Hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni; Neno hili limetoka kwa Bwana, Nalo ni ajabu machoni petu? 43 Kwa sababu hiyo nawaambia, Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa lingine lenye kuzaa matunda yake. 44 Naye aangukaye juu ya jiwe hilo atavunjika-vunjika; naye ye yote ambaye litamwangukia, litamsaga tikitiki. 45 Wakuu wa makuhani na Mafarisayo, waliposikia mifano yake, walitambua ya kuwa anawanenea wao. 46 Nao walipotafuta kumkamata, waliwaogopa makutano, kwa maana wao walimwona kuwa nabii.

Mathayo 22

1 Yesu akajibu, akawaambia tena kwa mithali, akisema, 2 Ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyemfanyia mwanawe arusi. 3 Akawatuma watumwa wake wawaite walioalikwa kuja arusini; nao wakakataa kuja. 4 Akatuma tena watu kwa wengine, akisema, Waambieni wale walioalikwa, Tazameni, nimeandaa karamu yangu; ng'ombe zangu na vinono vimekwisha kuchinjwa, na vyote vimekuwa tayari, njoni arusini. 5 Lakini hawakujali, wakaenda zao, mmoja shambani kwake, mmoja kwenye biashara yake; 6 nao waliosalia wakawakamata watumwa wake, wakawatenda jeuri, na kuwaua. 7 Basi yule mfalme akaghadhibika; akapeleka majeshi yake, akawaangamiza wauaji wale, akauteketeza mji wao. 8 Kisha akawaambia watumwa wake, Arusi i tayari, lakini wale walioalikwa hawakustahili. 9 Basi enendeni hata njia panda za barabara, na wote mwaonao waiteni arusini. 10 Watumwa wale wakatoka wakaenda njia kuu, wakakusanya wote waliowaona, waovu kwa wema; arusi ikajaa wageni. 11 Lakini alipoingia yule mfalme ili kuwatazama wageni wake, akaona mle mtu mmoja asiyevaa vazi la arusi. 12 Akamwambia, Rafiki, uliingiaje humu nawe huna vazi la arusi? Naye akatekewa. 13 Mfalme akawaambia watumishi, Mfungeni mikono na miguu, mchukueni mkamtupe katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. 14 Kwa maana waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache. 15 Ndipo Mafarisayo wakaenda zao, wakafanya shauri, jinsi ya kumtega kwa maneno. 16 Wakatuma kwake wanafunzi wao pamoja na Maherodi, wakasema, Mwalimu, twajua ya kuwa wewe u mtu wa kweli, na njia ya Mungu waifundisha katika kweli, wala hujali cheo cha mtu awaye yote, kwa maana hutazami sura za watu. 17 Basi utuambie, Waonaje? Ni halali kumpa Kaisari kodi, ama sivyo? 18 Lakini Yesu akaufahamu uovu wao, akasema, Mbona mnanijaribu, enyi wanafiki? 19 Nionyesheni fedha ya kodi. Nao wakamletea dinari. 20 Akawaambia, Ni ya nani sanamu hii, na anwani hii? 21 Wakamwambia, Ni ya Kaisari. Akawaambia, Basi, mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu. 22 Waliposikia, walistaajabu, wakamwacha, wakaenda zao. 23 Siku ile Masadukayo, watu wasemao ya kwamba hakuna kiyama, wakamwendea, wakamwuliza, 24 wakisema, Mwalimu, Musa alisema, Mtu akifa, akiwa hana watoto, ndugu yake na amwoe yule mkewe, ili ampatie nduguye mzao. 25 Basi, kwetu kulikuwa na ndugu saba; wa kwanza akaoa, akafariki, na kwa kuwa hana mzao, akamwachia nduguye mke wake. 26 Vivyo hivyo wa pili naye, na wa tatu, hata wote saba. 27 Mwisho wa wote yule mwanamke akafa naye. 28 Basi, katika kiyama, atakuwa mke wa yupi katika wale saba? Maana wote walikuwa naye. 29 Yesu akajibu, akawaambia, Mwapotea, kwa kuwa hamyajui maandiko wala uweza wa Mungu. 30 Kwa maana katika kiyama hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika mbinguni. 31 Tena kwa habari ya kiyama ya watu, hamjalisoma neno lililonenwa na Mungu, akisema, 32 Mimi ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? Mungu si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. 33 Na makutano waliposikia, walishangaa kwa mafunzo yake. 34 Na Mafarisayo waliposikia ya kwamba amewafumba kinywa wale Masadukayo, walifanya shauri pamoja. 35 Mmoja wao, mwana-sheria, akamwuliza, akimjaribu; 36 Mwalimu, katika torati ni amri ipi iliyo kuu? 37 Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. 38 Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. 39 Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. 40 Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii. 41 Na Mafarisayo walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mwaonaje katika habari za Kristo? 42 Ni mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. 43 Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi katika Roho kumwita Bwana, akisema, 44 Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwawekapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako? 45 Basi, Daudi akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? 46 Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala hakuthubutu mtu ye yote tangu siku ile kumwuliza neno tena.

Mathayo 23

1 Kisha Yesu akawaambia makutano na wanafunzi wake, akasema, 2 Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; 3 basi, yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi. 4 Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao. 5 Tena matendo yao yote huyatenda ili kutazamwa na watu; kwa kuwa hupanua hirizi zao, huongeza matamvua yao; 6 hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi, 7 na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi. 8 Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. 9 Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. 10 Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. 11 Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu. 12 Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa. 13 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie. 14 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnakula nyumba za wajane, na kwa unafiki mnasali sala ndefu; kwa hiyo mtapata hukumu iliyo kubwa zaidi. 15 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanum mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe. 16 Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga. 17 Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo kubwa, ile dhahabu, au lile hekalu liitakasalo dhahabu? 18 Tena, Mtu atakayeapa kwa madhabahu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa sadaka iliyo juu yake, amejifunga. 19 Vipofu ninyi; maana ni ipi iliyo kubwa, ile sadaka, au ile madhabahu iitakasayo sadaka? 20 Basi yeye aapaye kwa madhabahu, huapa kwa hiyo, na kwa vitu vyote vilivyo juu yake. 21 Naye aapaye kwa hekalu, huapa kwa hilo, na kwa yeye akaaye ndani yake. 22 Naye aapaye kwa mbingu, huapa kwa kiti cha enzi cha Mungu, na kwa yeye aketiye juu yake. 23 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache. 24 Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia. 25 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi. 26 Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi. 27 Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote. 28 Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi. 29 Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnayajenga makaburi ya manabii, na kuyapamba maziara ya wenye haki, 30 na kusema, Kama sisi tungalikuwako zamani za baba zetu, hatungalishirikiana nao katika damu ya manabii. 31 Hivi mwajishuhudia wenyewe, ya kwamba ninyi ni wana wao waliowaua manabii. 32 Kijazeni basi kipimo cha baba zenu. 33 Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya jehanum? 34 Kwa sababu hiyo, angalieni, mimi natuma kwenu manabii na wenye hekima na waandishi; na wengine wao ninyi mtawaua na kuwasulibisha, na wengine wao mtawapiga katika masinagogi yenu, na kuwafukuza mji kwa mji; 35 hivyo ije juu yenu damu yote ya haki iliyomwagika juu ya nchi, tangu damu ya Habili, yule mwenye haki, hata damu ya Zakaria bin Barakia, mliyemwua kati ya patakatifu na madhabahu. 36 Amin, nawaambieni, Mambo hayo yote yatakuja juu ya kizazi hiki. 37 Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! 38 Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa. 39 Kwa maana nawaambia, Hamtaniona kamwe tangu sasa, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana.

Mathayo 24

1 Yesu akaenda zake, akatoka hekaluni; wanafunzi wake wakamwendea ili kumwonyesha majengo ya hekalu. 2 Naye akajibu akawaambia, Hamyaoni haya yote? Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa. 3 Hata alipokuwa ameketi katika mlima wa Mizeituni, wanafunzi wake wakamwendea kwa faragha, wakisema, Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia? 4 Yesu akajibu, akawaambia, Angalieni, mtu asiwadanganye. 5 Kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi. 6 Nanyi mtasikia habari za vita na matetesi ya vita; angalieni, msitishwe; maana hayo hayana budi kutukia; lakini ule mwisho bado. 7 Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na matetemeko ya nchi mahali mahali. 8 Hayo yote ndiyo mwanzo wa utungu. 9 Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu. 10 Ndipo wengi watakapojikwaa, nao watasalitiana, na kuchukiana. 11 Na manabii wengi wa uongo watatokea, na kudanganya wengi. 12 Na kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa. 13 Lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka. 14 Tena habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja. 15 Basi hapo mtakapoliona chukizo la uharibifu, lile lililonenwa na nabii Danieli, limesimama katika patakatifu (asomaye na afahamu), 16 ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani; 17 naye aliye juu ya dari asishuke kuvichukua vitu vilivyomo nyumbani mwake; 18 wala aliye shambani asirudi nyuma kuichukua nguo yake. 19 Ole wao wenye mimba na wanyonyeshao siku hizo! 20 Ombeni, ili kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi, wala siku ya sabato. 21 Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. 22 Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo. 23 Wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule msisadiki. 24 Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule. 25 Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele. 26 Basi wakiwaambia, Yuko jangwani, msitoke; yumo nyumbani, msisadiki. 27 Kwa maana kama vile umeme utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi, hivyo ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. 28 Kwa kuwa po pote ulipo mzoga, ndipo watakapokusanyika tai. 29 Lakini mara, baada ya dhiki ya siku zile, jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wake, na nyota zitaanguka mbinguni, na nguvu za mbinguni zitatikisika; 30 ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi. 31 Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu. 32 Basi kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno u karibu; 33 nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. 34 Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia. 35 Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe. 36 Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake. 37 Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. 38 Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, 39 wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. 40 Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa; 41 wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa. 42 Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. 43 Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa. 44 Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja. 45 Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? 46 Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. 47 Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote. 48 Lakini mtumwa yule mbaya akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia; 49 akaanza kuwapiga wajoli wake, na kula na kunywa pamoja na walevi; 50 bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani, na saa asiyojua, 51 atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wanafiki; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

Mathayo 25

1 Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. 2 Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara. 3 Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; 4 bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. 5 Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. 6 Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. 7 Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. 8 Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika. 9 Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie. 10 Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa. 11 Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. 12 Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi. 13 Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa. 14 Maana ni mfano wa mtu atakaye kusafiri, aliwaita watumwa wake, akaweka kwao mali zake. 15 Akampa mmoja talanta tano, na mmoja talanta mbili, na mmoja talanta moja; kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake; akasafiri. 16 Mara yule aliyepokea talanta tano akaenda, akafanya biashara nazo, akachuma faida talanta nyingine tano. 17 Vile vile na yule mwenye mbili, yeye naye akachuma nyingine mbili faida. 18 Lakini yule aliyepokea moja alikwenda akafukua chini, akaificha fedha ya bwana wake. 19 Baada ya siku nyingi akaja bwana wa watumwa wale, akafanya hesabu nao. 20 Akaja yule aliyepokea talanta tano, akaleta talanta nyingine tano, akisema, Bwana, uliweka kwangu talanta tano; tazama, talanta nyingine tano nilizopata faida. 21 Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako. 22 Akaja na yule aliyepokea talanta mbili, akasema, Bwana, uliweka kwangu talanta mbili; tazama, talanta nyingine mbili nilizopata faida. 23 Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako. 24 Akaja na yule aliyepokea talanta moja, akasema, Bwana, nalitambua ya kuwa wewe u mtu mgumu, wavuna usipopanda, wakusanya usipotawanya; 25 basi nikaogopa, nikaenda nikaificha talanta yako katika ardhi; tazama, unayo iliyo yako. 26 Bwana wake akajibu, akamwambia, Wewe mtumwa mbaya na mlegevu, ulijua ya kuwa navuna nisipopanda, nakusanya nisipotawanya; 27 basi, ilikupasa kuiweka fedha yangu kwa watoao riba; nami nikija ningalipata iliyo yangu na faida yake. 28 Basi, mnyang'anyeni talanta hiyo, mpeni yule aliye nazo talanta kumi. 29 Kwa maana kila mwenye kitu atapewa, na kuongezewa tele; lakini asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa. 30 Na mtumwa yule asiyefaa, mtupeni mbali katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. 31 Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; 32 na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; 33 atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto. 34 Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu; 35 kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; 36 nalikuwa uchi, mkanivika nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. 37 Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? 38 Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? 39 Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? 40 Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi. 41 Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake; 42 kwa maana nalikuwa na njaa, msinipe chakula; nalikuwa na kiu, msininyweshe; 43 nalikuwa mgeni, msinikaribishe; nalikuwa uchi, msinivike; nalikuwa mgonjwa, na kifungoni, msije kunitazama. 44 Ndipo hao pia watajibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa, au una kiu, au u mgeni, au u uchi, au u mgonjwa, au u kifungoni, tusikuhudumie? 45 Naye atawajibu, akisema, Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi. 46 Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele.

Mathayo 26

1 Ikawa Yesu alipomaliza maneno hayo yote, aliwaambia wanafunzi wake, 2 Mnajua ya kuwa baada ya siku mbili itakuwa Pasaka, na Mwana wa Adamu atasalitiwa asulibiwe. 3 Wakati ule wakuu wa makuhani, na wazee wa watu, wakakusanyika katika behewa ya Kuhani Mkuu, jina lake Kayafa; 4 wakafanya shauri pamoja, ili wamkamate Yesu kwa hila na kumwua. 5 Lakini wakasema, Isiwe wakati wa sikukuu, isije ikatokea ghasia katika watu. 6 Naye Yesu alipokuwapo Bethania katika nyumba ya Simoni mkoma, 7 mwanamke mwenye kibweta cha marhamu ya thamani kubwa alimkaribia akaimimina kichwani pake alipoketi chakulani. 8 Wanafunzi wake walipoona, wakachukiwa, wakasema, Ni wa nini upotevu huu? 9 Maana marhamu hii ingaliweza kuuzwa kwa fedha nyingi wakapewa maskini. 10 Yesu akatambua akawaambia, Mbona mnamtaabisha mwanamke? Maana ni kazi njema aliyonitendea mimi. 11 Kwa maana siku zote mnao maskini pamoja nanyi; lakini mimi hamnami siku zote. 12 Maana kwa kunimwagia mwili wangu marhamu hiyo, ametenda hivyo ili kuniweka tayari kwa maziko yangu. 13 Amin, nawaambieni, Kila patakapohubiriwa Injili hii katika ulimwengu wote, tendo hilo alilolitenda huyu litatajwa pia kwa kumbukumbu lake. 14 Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, 15 akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. 16 Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti. 17 Hata siku ya kwanza ya mikate isiyotiwa chachu, wanafunzi wake wakamwendea Yesu, wakamwambia, Ni wapi utakapo tukuandalie uile Pasaka? 18 Akasema, Enendeni mjini kwa mtu fulani, mkamwambie, Mwalimu asema, Majira yangu ni karibu; kwako nitafanya Pasaka pamoja na wanafunzi wangu. 19 Wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, wakaiandaa Pasaka. 20 Basi kulipokuwa jioni aliketi chakulani pamoja na wale Thenashara. 21 Nao walipokuwa wakila, alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti. 22 Wakahuzunika sana, wakaanza kumwuliza mmoja mmoja, Ni mimi, Bwana? 23 Akajibu akasema, Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika kombe, ndiye atakayenisaliti. 24 Mwana wa Adamu aenda zake, kama alivyoandikiwa; lakini ole wake mtu yule ambaye amsaliti Mwana wa Adamu! Ingekuwa heri kwake mtu yule kama asingalizaliwa. 25 Yuda, yule mwenye kumsaliti, akajibu, akasema, Ni mimi, Rabi? Akamwambia, Wewe umesema. 26 Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu 27 Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki; 28 kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. 29 Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu. 30 Nao walipokwisha kuimba, wakatoka nje kwenda mlima wa Mizeituni. 31 Ndipo Yesu akawaambia, Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika. 32 Lakini baada ya kufufuka kwangu, nitawatangulia kwenda Galilaya. 33 Petro akajibu, akamwambia, Wajapochukizwa wote kwa ajili yako, mimi sitachukizwa kamwe. 34 Yesu akamwambia, Amin, nakuambia wewe, usiku huu kabla ya kuwika jogoo, utanikana mara tatu. 35 Petro akamwambia, Ijaponipasa kufa nawe, sitakukana kamwe. Na wanafunzi wote wakasema vivyo hivyo. 36 Kisha Yesu akaenda pamoja nao mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa, hata niende kule nikaombe. 37 Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka. 38 Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami. 39 Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe. 40 Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja? 41 Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu. 42 Akaenda tena mara ya pili, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwa haiwezekani kikombe hiki kiniepuke nisipokunywa, mapenzi yako yatimizwe. 43 Akaja tena, akawakuta wamelala; maana macho yao yamekuwa mazito. 44 Akawaacha tena, akaenda, akaomba mara ya tatu, akisema maneno yale yale. 45 Kisha akawajia wanafunzi wake, akawaambia, Laleni sasa, mpumzike tazama, saa imekaribia, na Mwana wa Adamu anatiwa katika mikono ya wenye dhambi. 46 Ondokeni, twende zetuni! Tazama, yule anayenisaliti amekaribia. 47 Basi alipokuwa katika kusema, tazama, Yuda, mmoja wa wale Thenashara akaja, na pamoja naye kundi kubwa wenye panga na marungu, wametoka kwa wakuu wa makuhani na wazee wa watu. 48 Na yule mwenye kumsaliti alikuwa amewapa ishara, akisema, Nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni. 49 Mara akamwendea Yesu, akasema, Salamu, Rabi, akambusu. 50 Yesu akamwambia, Rafiki, fanya ulilolijia. Wakaenda, wakanyosha mikono yao wakamkamata Yesu. 51 Na tazama, mmoja wao waliokuwa pamoja na Yesu akanyosha mkono wake, akaufuta upanga wake, akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio. 52 Ndipo Yesu akamwambia, Rudisha upanga wako mahali pake, maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga. 53 Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika? 54 Yatatimizwaje basi maandiko, ya kwamba hivyo ndivyo vilivyopasa kujiri? 55 Saa ile Yesu akawaambia makutano, Je, mmetoka kama kumkamata mnyang'anyi, wenye panga na marungu, ili kunishika? Kila siku naliketi hekaluni nikifundisha, msinikamate. 56 Lakini haya yote yamekuwa, ili maandiko ya manabii yatimizwe. Ndipo wanafunzi wote wakamwacha, wakakimbia. 57 Nao waliomkamata Yesu wakampeleka kwa Kayafa, Kuhani Mkuu, walikokuwa wamekutanika waandishi na wazee. 58 Na Petro akamfuata kwa mbali mpaka behewa ya Kuhani Mkuu, akaingia ndani, akaketi pamoja na watumishi, auone mwisho. 59 Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda wa uongo juu ya Yesu, wapate kumwua; 60 wasiuone wangawa walitokea mashahidi wa uongo wengi. 61 Hata baadaye wawili wakatokea, wakasema, Huyu alisema, Naweza kulivunja hekalu la Mungu, na kulijenga kwa siku tatu. 62 Kisha Kuhani Mkuu akasimama akamwambia, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? 63 Lakini, Yesu akanyamaza. Kuhani Mkuu akamwambia, Nakuapisha kwa Mungu aliye hai, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu. 64 Yesu akamwambia, Wewe umesema; lakini nawaambieni, Tangu sasa mtamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kuume wa nguvu, akija juu ya mawingu ya mbinguni. 65 Ndipo Kuhani Mkuu akararua mavazi yake, akisema, Amekufuru; mna haja gani tena ya mashahidi? Tazameni, sasa mmesikia hiyo kufuru yake; 66 mwaonaje ninyi? Wakajibu, wakasema, Imempasa kuuawa. 67 Ndipo wakamtemea mate ya uso, wakampiga makonde; wengine wakampiga makofi, 68 wakisema, Ewe Kristo, tufumbulie; ni nani aliyekupiga? 69 Na Petro alikuwa ameketi nje behewani; kijakazi mmoja akamwendea, akasema, Wewe nawe ulikuwapo pamoja na Yesu wa Galilaya. 70 Akakana mbele ya wote, akisema, Sijui usemalo. 71 Naye alipotoka nje hata ukumbini, mwanamke mwingine alimwona, akawaambia watu waliokuwako huko, Huyu alikuwapo pamoja na Yesu Mnazareti. 72 Akakana tena kwa kiapo, Simjui mtu huyu. 73 Punde kidogo, wale waliohudhuria wakamwendea, wakamwambia Petro, Hakika wewe nawe u mmoja wao; kwa sababu hata usemi wako wakutambulisha. 74 Ndipo akaanza kulaani na kuapa akisema, Simjui mtu huyu. Na mara akawika jogoo. 75 Petro akalikumbuka lile neno la Yesu alilolisema, Kabla ya kuwika jogoo, utanikana mara tatu. Akatoka nje, akalia kwa majonzi.

Mathayo 27

1 Na ilipokuwa asubuhi, wakuu wa makuhani wote na wazee wa watu wakafanya shauri juu ya Yesu, wapate kumwua; 2 wakamfunga, wakamchukua, wakampeleka kwa Pilato aliyekuwa liwali. 3 Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, alipoona ya kuwa amekwisha kuhukumiwa, alijuta, akawarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande thelathini vya fedha, akasema, Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia. 4 Wakasema, Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe. 5 Akavitupa vile vipande vya fedha katika hekalu, akaondoka; akaenda, akajinyonga. 6 Wakuu wa makuhani wakavitwaa vile vipande vya fedha, wakasema, Si halali kuviweka katika sanduku ya sadaka, kwa kuwa ni kima cha damu. 7 Wakafanya shauri, wakavitumia kwa kununua konde la mfinyanzi liwe mahali pa kuzika wageni. 8 Kwa hiyo konde lile huitwa konde la damu hata leo. 9 Ndipo likatimia neno lililonenwa na nabii Yeremia, akisema, Wakavitwaa vipande thelathini vya fedha, kima chake aliyetiwa kima, ambaye baadhi ya Waisraeli walimtia kima; 10 wakavitumia kwa kununua konde la mfinyanzi, kama Bwana alivyoniagiza. 11 Naye Yesu akasimama mbele ya liwali; liwali akamwuliza, akasema, Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi? Yesu akamwambia, Wewe wasema. 12 Lakini aliposhitakiwa na wakuu wa makuhani na wazee, hakujibu hata neno. 13 Ndipo Pilato akamwambia, Husikii ni mambo mangapi wanayokushuhudia? 14 Asimjibu hata neno moja, hata liwali akastaajabu sana. 15 Basi wakati wa siku kuu, liwali desturi yake huwafungulia mkutano mfungwa mmoja waliyemtaka. 16 Basi palikuwa na mfungwa mashuhuri siku zile, aitwaye Baraba. 17 Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? 18 Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda. 19 Na alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mkewe alimpelekea mjumbe, kumwambia, Usiwe na neno na yule mwenye haki; kwa sababu nimeteswa mengi leo katika ndoto kwa ajili yake. 20 Nao wakuu wa makuhani na wazee wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu. 21 Basi liwali akajibu, akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi katika hawa wawili? Wakasema, Baraba. 22 Pilato akawaambia, Basi, nimtendeje Yesu aitwaye Kristo? Wakasema wote, Asulibiwe. 23 Akasema, Kwani? Ni ubaya gani alioutenda? Wakazidi sana kupiga kelele, wakisema, Na asulibiwe. 24 Basi Pilato alipoona ya kuwa hafai lo lote, bali ghasia inazidi tu, akatwaa maji, akanawa mikono yake mbele ya mkutano, akasema, Mimi sina hatia katika damu ya mtu huyu mwenye haki; yaangalieni haya ninyi wenyewe. 25 Watu wote wakajibu wakasema, Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu. 26 Ndipo akawafungulia Baraba; na baada ya kumpiga Yesu mijeledi, akamtoa ili asulibiwe. 27 Ndipo askari wa liwali wakamchukua Yesu ndani ya Praitorio, wakamkusanyikia kikosi kizima. 28 Wakamvua nguo, wakamvika vazi jekundu. 29 Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! 30 Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. 31 Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha. 32 Hata walipokuwa wakitoka, wakamwona mtu Mkirene, jina lake Simoni; huyu wakamshurutisha auchukue msalaba wake. 33 Na walipofika mahali paitwapo Golgotha, yaani, Fuvu la kichwa, 34 wakampa kunywa divai iliyochanganyika na nyongo; lakini yeye alipoionja hakutaka kunywa. 35 Walipokwisha kumsulibisha, waligawa mavazi yake, wakipiga kura; ili litimie neno lililonenwa na nabii, Waligawa nguo zangu kati yao, na juu ya vazi langu walipiga kura. 36 Wakaketi, wakamlinda huko. 37 Wakaweka juu ya kichwa chake mashitaka yake, yaliyoandikwa HUYU NI YESU, MFALME WA WAYAHUDI. 38 Wakati uo huo wanyang'anyi wawili wakasulibiwa pamoja naye, mmoja mkono wake wa kuume, na mmoja mkono wake wa kushoto. 39 Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, 40 Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani. 41 Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. 42 Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. 43 Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu. 44 Pia wale wanyang'anyi waliosulibiwa pamoja naye walimshutumu vile vile. 45 Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. 46 Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? 47 Na baadhi yao waliohudhuria, waliposikia, walisema, Huyu anamwita Eliya. 48 Mara mmoja wao akaenda mbio, akatwaa sifongo, akaijaza siki, akaitia juu ya mwanzi, akamnywesha. 49 Wale wengine wakasema, Acha; na tuone kama Eliya anakuja kumwokoa. 50 Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. 51 Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka; 52 makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; 53 nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi. 54 Basi yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu. 55 Palikuwa na wanawake wengi pale wakitazama kwa mbali, hao ndio waliomfuata Yesu toka Galilaya, na kumtumikia. 56 Miongoni mwao alikuwamo Mariamu Magdalene, na Mariamu mama yao Yakobo na Yusufu, na mama yao wana wa Zebedayo. 57 Hata ilipokuwa jioni akafika mtu tajiri wa Arimathaya, jina lake Yusufu, naye mwenyewe alikuwa mwanafunzi wa Yesu; 58 mtu huyu alimwendea Pilato akauomba mwili wa Yesu. Ndipo Pilato akaamuru apewe. 59 Yusufu akautwaa mwili, akauzonga-zonga katika sanda ya kitani safi, 60 akauweka katika kaburi lake jipya, alilokuwa amelichonga mwambani; akavingirisha jiwe kubwa mbele ya mlango wa kaburi, akaenda zake. 61 Na pale walikuwapo Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, wameketi kulielekea kaburi. 62 Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, 63 wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. 64 Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. 65 Pilato akawaambia, Mna askari; nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. 66 Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.

Mathayo 28

1 Hata sabato ilipokwisha, ikipambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. 2 Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia. 3 Na sura yake ilikuwa kama umeme, na mavazi yake meupe kama theluji. 4 Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu. 5 Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi; kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. 6 Hayupo hapa; kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. 7 Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda Galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia. 8 Wakaondoka upesi kutoka kaburini, kwa hofu na furaha nyingi, wakaenda mbio kuwapasha wanafunzi wake habari. 9 Na tazama, Yesu akakutana nao, akisema, Salamu! Wakakaribia wakamshika miguu, wakamsujudia. 10 Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona. 11 Nao wale walipokuwa wakienda, tazama, baadhi ya askari waliingia mjini, wakawapasha wakuu wa makuhani habari za mambo yote yaliyotendeka. 12 Wakakusanyika pamoja na wazee, wakafanya shauri, wakawapa askari fedha nyingi, 13 wakisema, Semeni, ya kwamba wanafunzi wake walikuja usiku, wakamwiba, sisi tulipokuwa tumelala. 14 Na neno hili likisikilikana kwa liwali, sisi tutasema naye, nanyi tutawaondolea wasiwasi. 15 Basi wakazitwaa zile fedha, wakafanya kama walivyofundishwa. Na neno hilo likaenea kati ya Wayahudi hata leo. 16 Na wale wanafunzi kumi na mmoja wakaenda Galilaya mpaka mlima ule aliowaagiza Yesu. 17 Nao walipomwona, walimsujudia; lakini baadhi yao waliona shaka. 18 Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. 19 Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; 20 na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.

Marko 1

1 Mwanzo wa Injili ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. 2 Kama ilivyoandikwa katika nabii Isaya, Tazama, namtuma mjumbe wangu Mbele ya uso wako, Atakayeitengeneza njia yako. 3 Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake. 4 Yohana alitokea, akibatiza nyikani, na kuuhubiri ubatizo wa toba liletalo ondoleo la dhambi. 5 Wakamwendea nchi yote ya Uyahudi, nao wa Yerusalemu wote, wakabatizwa katika mto wa Yordani, wakiziungama dhambi zao. 6 Na Yohana alikuwa amevaa singa za ngamia na mshipi wa ngozi kiunoni mwake, akala nzige na asali ya mwitu. 7 Akahubiri akisema, Yuaja nyuma yangu aliye na nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuinama na kuilegeza gidamu ya viatu vyake. 8 Mimi niliwabatiza kwa maji; bali yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu. 9 Ikawa siku zile, Yesu alikuja kutoka Nazareti ya Galilaya, akabatizwa na Yohana katika Yordani. 10 Mara alipopanda kutoka majini, akaona mbingu zinapasuka, na Roho, kama hua, akishuka juu yake; 11 na sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe. 12 Mara Roho akamtoa aende nyikani. 13 Akawako huko jangwani siku arobaini, hali akijaribiwa na Shetani; naye alikuwa pamoja na wanyama wa mwitu, na malaika walikuwa wakimhudumia. 14 Hata baada ya Yohana kutiwa gerezani, Yesu akaenda Galilaya, akiihubiri Habari Njema ya Mungu, 15 akisema, Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili. 16 Naye alipokuwa akipita kando ya bahari ya Galilaya, akamwona Simoni na Andrea nduguye, wakitupa jarife baharini; kwa maana walikuwa wavuvi. 17 Yesu akawaambia, Njoni mnifuate, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu. 18 Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. 19 Akaendelea mbele kidogo, akamwona Yakobo wa Zebedayo, na Yohana nduguye, nao pia walikuwa chomboni, wakizitengeneza nyavu zao. 20 Mara akawaita, wakamwacha baba yao Zebedayo ndani ya chombo pamoja na watu wa mshahara, wakaenda, wakamfuata. 21 Wakashika njia mpaka Kapernaumu, na mara siku ya sabato akaingia katika sinagogi, akafundisha. 22 Wakashangaa mno kwa mafundisho yake; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi. 23 Na mara palikuwapo ndani ya sinagogi lao mtu mwenye pepo mchafu; akapaza sauti, 24 akisema, Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Je! Umekuja kutuangamiza? 25 Nakutambua u nani, Mtakatifu wa Mungu. Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, umtoke. 26 Yule pepo mchafu akamtia kifafa, akalia kwa sauti kuu, akamtoka. 27 Wakashangaa wote, hata wakaulizana, wakisema, Nini hii? Ni elimu mpya! Maana kwa uweza awaamuru hata pepo wachafu, nao wamtii! 28 Habari zake zikaenea mara kotekote katika nchi zote kandokando ya Galilaya. 29 Na mara walipotoka katika sinagogi, walifika nyumbani kwa Simoni na Andrea, pamoja na Yakobo na Yohana. 30 Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia habari zake. 31 Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia. 32 Hata kulipokuwa jioni, na jua limekwisha kuchwa, walikuwa wakimletea wote waliokuwa hawawezi, na wenye pepo. 33 Na mji wote ulikuwa umekusanyika mlangoni. 34 Akaponya wengi waliokuwa na maradhi mbalimbali, akatoa pepo wengi, wala hakuwaacha pepo kunena, kwa sababu walimjua. 35 Hata alfajiri na mapema sana akaondoka, akatoka akaenda zake mahali pasipokuwa na watu, akaomba huko. 36 Simoni na wenziwe wakamfuata; 37 nao walipomwona wakamwambia, Watu wote wanakutafuta. 38 Akawaambia, Twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea. 39 Akaenda akihubiri katika masinagogi yao, katika nchi yote ya Galilaya, na kutoa pepo. 40 Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa. 41 Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. 42 Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika. 43 Akamkataza kwa nguvu, akamwondoa mara, 44 akamwambia, Angalia, usimwambie mtu neno lolote, ila enenda zako ukajionyeshe kwa kuhani, ukatoe alivyoamuru Musa kwa kutakasika kwako, iwe ushuhuda kwao. 45 Lakini akatoka, akaanza kuhubiri maneno mengi, na kulitangaza lile neno, hata Yesu asiweze tena kuingia mjini kwa wazi; bali alikuwako nje mahali pasipokuwa na watu, wakamwendea kutoka kila mahali.

Marko 2

1 Akaingia Kapernaumu tena, baada ya siku kadha wa kadha, ikasikiwa ya kwamba yumo nyumbani. 2 Wakakusanyika watu wengi, isibaki nafasi hata mlangoni; akawa akisema nao neno lake. 3 Wakaja watu wakimletea mtu mwenye kupooza, anachukuliwa na watu wanne. 4 Na walipokuwa hawawezi kumkaribia kwa sababu ya makutano, waliitoboa dari pale alipokuwapo; na wakiisha kuivunja wakalitelemsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza. 5 Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako. 6 Na baadhi ya waandishi walikuwako huko, wameketi, wakifikiri mioyoni mwao, 7 Mbona huyu anasema hivi? Anakufuru. Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa mmoja, ndiye Mungu? 8 Mara Yesu akafahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao, akawaambia, Mbona mnafikiri hivi mioyoni mwenu? 9 Vyepesi ni vipi, kumwambia mwenye kupooza, Umesamehewa dhambi zako, au kusema, Ondoka, ujitwike godoro lako, uende? 10 Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (hapo amwambia yule mwenye kupooza), 11 Nakuambia, Ondoka, ujitwike godoro lako uende nyumbani kwako. 12 Mara akaondoka, akajitwika godoro lake, akatoka mbele yao wote; hata wakastaajabu wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Namna hii hatujapata kuiona kamwe. 13 Akatoka tena, akaenda kando ya bahari, mkutano wote ukamwendea, akawafundisha. 14 Hata alipokuwa akipita, akamwona Lawi wa Alfayo, ameketi forodhani, akamwambia, Nifuate. Akaondoka akamfuata. 15 Hata alipokuwa ameketi chakulani nyumbani mwake, watoza ushuru wengi na wenye dhambi waliketi pamoja na Yesu na wanafunzi wake; kwa maana walikuwa wengi wakimfuata. 16 Na waandishi na Mafarisayo walipomwona anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi, waliwaambia wanafunzi wake, Mbona anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? 17 Yesu aliposikia aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi; sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi. 18 Nao wanafunzi wake Yohana na Mafarisayo walikuwa wakifunga; basi walikuja, wakamwambia, Kwani wanafunzi wa Yohana na wanafunzi wa Mafarisayo hufunga, bali wanafunzi wako hawafungi? 19 Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kufunga maadamu bwana-arusi yupo pamoja nao? Muda wote walipo na bwana-arusi pamoja nao hawawezi kufunga. 20 Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana-arusi, ndipo watakapofunga siku ile. 21 Hakuna mtu ashonaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; ikiwa ashona, kile kipya kilichotiwa huliharibu lile vazi kuukuu, na pale palipotatuka huzidi. 22 Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; ikiwa atia, ile divai mpya itavipasua viriba vile, divai ikamwagika, vile viriba vikaharibika. Bali hutia divai mpya katika viriba vipya. 23 Ikawa alipokuwa akipita mashambani siku ya sabato, wanafunzi wake walianza kuendelea njiani wakivunja masuke. 24 Mafarisayo wakamwambia, Tazama, mbona wanafanya lisilokuwa halali siku ya sabato? 25 Akawaambia, Hamkusoma popote alivyofanya Daudi, alipokuwa ana haja, na kuona njaa, yeye na wenziwe? 26 Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, zamani za kuhani mkuu Abiathari, akaila mikate ile ya Wonyesho, ambayo si halali kuliwa ila na makuhani, akawapa na wenziwe? 27 Akawaambia, Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu, si mwanadamu kwa ajili ya sabato. 28 Basi Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato pia.

Marko 3

1 Akaingia tena katika sinagogi; na palikuwako huko mtu mwenye mkono uliopooza; 2 wakamvizia ili kuona kama atamponya siku ya sabato; wapate kumshitaki. 3 Akamwambia yule mtu mwenye mkono uliopooza, Simama katikati. 4 Akawauliza, Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya? Kuponya roho au kuiua? Wakanyamaza. 5 Akawakazia macho pande zote kwa hasira, akiona huzuni kwa ajili ya ugumu wa mioyo yao, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Naye akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena. 6 Mara wakatoka wale Mafarisayo, wakawa wakifanya shauri juu yake pamoja na Maherodi, jinsi ya kumwangamiza. 7 Naye Yesu akajitenga, yeye na wanafunzi wake, akaenda baharini. Mkutano mkuu ukamfuata, kutoka Galilaya, na Uyahudi, 8 na Yerusalemu, na Idumaya, na ng'ambo ya Yordani, na pande za Tiro na Sidoni, mkutano mkuu, waliposikia habari za mambo yote aliyokuwa akiyatenda, wakamwendea. 9 Akawaambia wanafunzi wake ya kwamba chombo kidogo kikae karibu naye, kwa sababu ya mkutano, wasije wakamsonga. 10 Maana aliponya wengi, hata wote waliokuwa na misiba wakamrukia wapate kumgusa. 11 Na pepo wachafu, kila walipomwona, walianguka mbele yake, wakalia wakisema, Wewe ndiwe Mwana wa Mungu. 12 Akawakataza sana, wasimdhihirishe. 13 Akapanda mlimani, akawaita aliowataka mwenyewe; wakamwendea. 14 Akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, 15 tena wawe na amri ya kutoa pepo. 16 Akawaweka wale Thenashara; na Simoni akampa jina la Petro; 17 na Yakobo, mwana wa Zebedayo, na Yohana nduguye Yakobo, akawapa jina la Boanerge, maana yake, wana wa ngurumo; 18 na Andrea, na Filipo, na Bartholomayo, na Mathayo, na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Thadayo, na Simoni Mkananayo, 19 na Yuda Iskariote, ndiye aliyemsaliti. Kisha akaingia nyumbani. 20 Mkutano wakakusanyika tena, hata wao wenyewe wasiweze hata kula mkate. 21 Jamaa zake walipopata habari wakatoka kwenda kumkamata; maana walisema, Amerukwa na akili. 22 Nao waandishi walioshuka kutoka Yerusalemu wakasema, Ana Beelzebuli, na, Kwa mkuu wa pepo huwatoa pepo. 23 Akawaita, akawaambia kwa mifano, Awezaje Shetani kumtoa Shetani? 24 Na ufalme ukifitinika juu ya nafsi yake, ufalme huo hauwezi kusimama; 25 na nyumba ikifitinika juu ya nafsi yake, nyumba hiyo haiwezi kusimama. 26 Na kama Shetani ameondoka juu ya nafsi yake, akafitinika, hawezi kusimama, bali huwa na kikomo. 27 Hawezi mtu kuingia ndani ya nyumba ya mtu mwenye nguvu, na kuviteka vitu vyake, asipomfunga kwanza yule mwenye nguvu; ndipo atakapoiteka nyumba yake. 28 Amin, nawaambia, Dhambi zote watasamehewa wanadamu, na kufuru zao watakazokufuru zote; 29 bali mtu atakayemkufuru Roho Mtakatifu hana msamaha hata milele; ila atakuwa ana dhambi ya milele, 30 kwa vile walivyosema, Ana pepo mchafu. 31 Wakaja mamaye na nduguze; wakasimama nje, wakatuma mtu kumwita. 32 Na makutano walikuwa wameketi, wakimzunguka, wakamwambia, Tazama, mama yako na ndugu zako wako nje, wanakutafuta. 33 Akawajibu, akisema, Mama yangu na ndugu zangu ni akina nani? 34 Akawatazama wale walioketi wakimzunguka pande zote, akasema, Tazama, mama yangu na ndugu zangu! 35 Kwa maana mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.

Marko 4

1 Akaanza kufundisha tena kando ya bahari. Wakamkusanyikia mkutano mkubwa mno, hata yeye akapanda chomboni, akakaa baharini, mkutano wote ulikuwako juu ya nchi kavu kando ya bahari. 2 Akawafundisha mambo mengi kwa mifano, akawaambia katika mafundisho yake, 3 Sikilizeni; Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda; 4 ikawa alipokuwa akipanda, mbegu nyingine ilianguka kando ya njia, wakaja ndege wakaila. 5 Nyingine ikaanguka penye mwamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara ikaota kwa kuwa na udongo haba; 6 hata jua lilipozuka iliungua, na kwa kuwa haina mizizi ikanyauka. 7 Nyingine ikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea ikaisonga, isizae matunda. 8 Nyingine zikaanguka penye udongo ulio mzuri, zikazaa matunda, zikimea na kukua, na kuzaa, moja thelathini, moja sitini, na moja mia. 9 Akasema, Aliye na masikio ya kusikilia, na asikie. 10 Naye alipokuwa peke yake, wale watu waliomzunguka, na wale Thenashara, walimwuliza habari za ile mifano. 11 Akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuijua siri ya ufalme wa Mungu, bali kwa wale walio nje yote hufanywa kwa mifano, 12 ili wakitazama watazame, wasione; Na wakisikia wasikie, wasielewe; Wasije wakaongoka, na kusamehewa. 13 Akawaambia, Hamjui mfano huu? Basi mifano yote mtaitambuaje? 14 Mpanzi huyo hulipanda neno. 15 Hawa ndio walio kando ya njia lipandwapo neno; nao, wakiisha kusikia, mara huja Shetani, akaliondoa lile neno lililopandwa mioyoni mwao. 16 Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; 17 ila hawana mizizi ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara hujikwaa. 18 Na hawa ndio wale wapandwao penye miiba; ni watu walisikiao lile neno, 19 na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai. 20 Na hawa ndio waliopandwa penye udongo ulio mzuri; ni watu walisikiao lile neno na kulipokea, na kuzaa matunda, mmoja thelathini, mmoja sitini, na mmoja mia. 21 Akawaambia, Mwaonaje? Taa huja ili kuwekwa chini ya pishi, au mvunguni? Si kuwekwa juu ya kiango? 22 Kwa maana hakuna neno lililositirika, ila makusudi lije likadhihirika; wala hakuna lililofichwa, ila makusudi lije likatokea wazi. 23 Mtu akiwa na masikio ya kusikilia, na asikie. 24 Akawaambia, Angalieni msikialo; kipimo kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa. 25 Kwa maana mwenye kitu atapewa, naye asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa. 26 Akasema, Ufalme wa Mungu, mfano wake ni kama mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi; 27 akawa akilala na kuondoka, usiku na mchana, nayo mbegu ikamea na kukua, asivyojua yeye. 28 Maana nchi huzaa yenyewe; kwanza jani, tena suke, kisha ngano pevu katika suke. 29 Hata matunda yakiiva, mara atapeleka mundu, kwa kuwa mavuno yamefika. 30 Akasema, Tuulinganishe na nini ufalme wa Mungu? Au tuutie katika mfano gani? 31 Ni kama punje ya haradali, ambayo ipandwapo katika nchi, ingawa ni ndogo kuliko mbegu zote zilizo katika nchi, 32 lakini ikiisha kupandwa hukua, ikawa kubwa kuliko miti yote ya mboga, ikafanya matawi makubwa; hata ndege wa angani waweza kukaa chini ya uvuli wake. 33 Kwa mifano mingi ya namna hii alikuwa akisema nao neno lake, kwa kadiri walivyoweza kulisikia; 34 wala pasipo mfano hakusema nao; lakini akawaeleza wanafunzi wake mwenyewe mambo yote kwa faragha. 35 Siku ile kulipokuwa jioni, akawaambia, Na tuvuke mpaka ng'ambo. 36 Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. 37 Ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. 38 Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia? 39 Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu. 40 Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado? 41 Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?

Marko 5

1 Wakafika ng'ambo ya bahari mpaka nchi ya Wagerasi. 2 Na alipokwisha kushuka chomboni, mara alikutana na mtu, ambaye ametoka makaburini, mwenye pepo mchafu; 3 makao yake yalikuwa pale makaburini; wala hakuna mtu ye yote aliyeweza kumfunga tena, hata kwa minyororo; 4 kwa sababu alikuwa amefungwa mara nyingi kwa pingu na minyororo, akaikata ile minyororo, na kuzivunja-vunja zile pingu; wala hakuna mtu aliyekuwa na nguvu za kumshinda. 5 Na sikuzote, usiku na mchana, alikuwako makaburini na milimani, akipiga kelele na kujikata-kata kwa mawe. 6 Na alipomwona Yesu kwa mbali, alipiga mbio, akamsujudia; 7 akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese. 8 Kwa sababu amemwambia, Ewe pepo mchafu, mtoke mtu huyu. 9 Akamwuliza, Jina lako nani? Akamjibu, Jina langu ni Legioni, kwa kuwa tu wengi. 10 Akamsihi sana asiwapeleke nje ya nchi ile. 11 Na hapo milimani palikuwa na kundi kubwa la nguruwe, wakilisha. 12 Pepo wote wakamsihi, wakisema, Tupeleke katika nguruwe, tupate kuwaingia wao. 13 Akawapa ruhusa. Wale pepo wachafu wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote likatelemka kwa kasi gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa baharini. 14 Wachungaji wao wakakimbia, wakaieneza habari mjini na mashambani. Watu wakatoka walione lililotokea. 15 Wakamwendea Yesu, wakamwona yule mwenye pepo, ameketi, amevaa nguo, ana akili zake, naye ndiye aliyekuwa na lile jeshi; wakaogopa. 16 Na wale waliokuwa wameona waliwaeleza ni mambo gani yaliyompata yule mwenye pepo, na habari za nguruwe. 17 Wakaanza kumsihi aondoke mipakani mwao. 18 Naye alipokuwa akipanda chomboni, yule aliyekuwa na pepo akamsihi kwamba awe pamoja naye; 19 lakini hakumruhusu, bali alimwambia, Enenda zako nyumbani kwako, kwa watu wa kwenu, kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu. 20 Akaenda zake, akaanza kuhubiri katika Dekapoli, ni mambo gani makuu Yesu aliyomtendea; watu wote wakastaajabu. 21 Hata Yesu alipokwisha kuvuka kurudia ng'ambo katika kile chombo, wakamkusanyikia mkutano mkuu; naye alikuwa kando ya bahari. 22 Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, 23 akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi. 24 Akaenda pamoja naye; mkutano mkuu wakamfuata, wakimsonga-songa. 25 Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, 26 na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya 27 aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; 28 maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona. 29 Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule. 30 Mara Yesu, hali akifahamu nafsini mwake kwamba nguvu zimemtoka, akageuka kati ya mkutano, akasema, Ni nani aliyenigusa mavazi yangu? 31 Wanafunzi wake wakamwambia, Je! Wawaona makutano wanavyokusonga-songa, nawe wasema, Ni nani aliyenigusa? 32 Akatazama pande zote ili amwone yule aliyelitenda neno hilo. 33 Na yule mwanamke akaingiwa na hofu na kutetemeka, akijua lililompata, akaja akamwangukia, akamweleza kweli yote. 34 Akamwambia, Binti, imani yako imekuponya, enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena. 35 Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? 36 Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. 37 Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo. 38 Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. 39 Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. 40 Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana. 41 Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. 42 Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana alikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. 43 Akawaonya sana, mtu asijue habari ile; akaamuru apewe chakula.

Marko 6

1 Akatoka huko, akafika mpaka nchi ya kwao; wanafunzi wake wakamfuata. 2 Na ilipokuwa sabato, alianza kufundisha katika sinagogi; wengi waliposikia wakashangaa, wakisema, Huyu ameyapata wapi haya? Na, Ni hekima gani hii aliyopewa huyu? Na, Ni nini miujiza hii mikubwa inayotendeka kwa mikono yake? 3 Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake. 4 Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake. 5 Wala hakuweza kufanya mwujiza wo wote huko, isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache, akawaponya. 6 Akastaajabu kwa sababu ya kutokuamini kwao. Akazunguka-zunguka katika vile vijiji, akifundisha. 7 Akawaita wale Thenashara, akaanza kuwatuma wawili wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu; 8 akawakataza wasichukue kitu cha njiani isipokuwa fimbo tu; wala mkate, wala mkoba, wala pesa za bindoni; 9 lakini wajifungie viatu; akasema, Msivae kanzu mbili. 10 Akawaambia, Mahali po pote mtakapoingia katika nyumba, kaeni humo hata mtakapotoka mahali pale. 11 Na mahali po pote wasipowakaribisha ninyi wala kuwasikia, mtokapo huko, yakung'uteni mavumbi yaliyo chini ya miguu yenu, kuwa ushuhuda kwao. 12 Wakatoka, wakahubiri kwamba watu watubu. 13 Wakatoa pepo wengi, wakapaka mafuta watu wengi waliokuwa wagonjwa, wakawapoza. 14 Naye Mfalme Herode akasikia habari; kwa maana jina lake lilikuwa kutangaa, akasema, Yohana Mbatizaji amefufuka katika wafu, na kwa hiyo nguvu hizi zinatenda kazi ndani yake. 15 Wengine walisema, Ni Eliya. Wengine walisema, Huyu ni nabii, au ni kama mmoja wa manabii. 16 Lakini Herode aliposikia, alisema, Yohana, niliyemkata kichwa, amefufuka. 17 Kwa maana Herode mwenyewe alikuwa ametuma watu, akamkamata Yohana, akamfunga gerezani, kwa ajili ya Herodia, mkewe Filipo ndugu yake, kwa kuwa amemwoa; 18 kwa sababu Yohana alimwambia Herode, Si halali kwako kuwa na mke wa nduguyo. 19 Naye yule Herodia akawa akimvizia, akataka kumwua, asipate. 20 Maana Herode alimwogopa Yohana; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana; naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha. 21 Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya; 22 ndipo binti yake yule Herodia alipoingia, akacheza, akampendeza Herode na wale walioketi pamoja naye karamuni. Mfalme akamwambia yule kijana, Niombe lo lote utakalo, nitakupa. 23 Akamwapia, Lo lote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu. 24 Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohana Mbatizaji. 25 Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, Nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji. 26 Mfalme akafanya huzuni sana, lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia. 27 Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake. Basi akaenda, akamkata kichwa mle gerezani, 28 akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye. 29 Wanafunzi wake waliposikia habari, walikwenda, wakauchukua mwili wake, wakauzika kaburini. 30 Na mitume wakakusanyika mbele ya Yesu; wakampa habari za mambo yote waliyoyafanya, na mambo yote waliyoyafundisha. 31 Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula. 32 Wakaenda zao faragha mashuani, mahali pasipokuwa na watu. 33 Watu wakawaona wakienda zao, na wengi wakatambua, wakaenda huko mbio kwa miguu, toka miji yote, wakatangulia kufika. 34 Naye aliposhuka mashuani, akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi. 35 Hata zilipopita saa nyingi za mchana, wanafunzi wake walimwendea, wakasema, Mahali hapa ni nyika tupu, na sasa kunakuchwa; 36 uwaage watu hawa, ili waende zao mashambani na vijijini kandokando, wakajinunulie chakula. 37 Akajibu, akawaambia, Wapeni ninyi chakula. Wakamwambia, Je! Twende tukanunue mikate ya dinari mia mbili ili tuwape kula? 38 Akawaambia, Mnayo mikate mingapi? Nendeni mkatazame. Walipokwisha kujua wakasema, Mitano, na samaki wawili. 39 Akawaagiza wawaketishe wote, vikao vikao, penye majani mabichi. 40 Wakaketi safu safu, hapa mia hapa hamsini. 41 Akaitwaa ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni, akashukuru, akaimega ile mikate, akawapa wanafunzi wake wawaandikie; na wale samaki wawili akawagawia wote. 42 Wakala wote wakashiba. 43 Wakaokota vipande vilivyomegwa vya kuweza kujaza vikapu kumi na viwili; na vipande vya samaki pia. 44 Na walioila ile mikate wapata elfu tano wanaume. 45 Mara akawalazimisha wanafunzi wake wapande mashuani, watangulie kwenda ng'ambo hata Bethsaida, wakati yeye alipokuwa akiwaaga mkutano. 46 Hata alipokwisha kuagana nao akaenda zake mlimani kuomba. 47 Na kulipokuwa jioni mashua ilikuwa katikati ya bahari, na yeye yu peke yake katika nchi kavu. 48 Akawaona wakitaabika kwa kuvuta makasia, kwa maana upepo ulikuwa wa mbisho; hata ilipopata kama zamu ya nne ya usiku akawaendea, akitembea juu ya bahari; akataka kuwapita. 49 Nao walipomwona anatembea juu ya bahari, walidhani ya kuwa ni kivuli, wakapiga yowe, 50 kwa kuwa wote walimwona, wakafadhaika. Mara akasema nao, akawaambia, Changamkeni; ni mimi, msiogope. 51 Akapanda mle chomboni walimo; upepo ukakoma; wakashangaa sana mioyoni mwao; 52 kwa maana hawakufahamu habari za ile mikate, lakini mioyo yao ilikuwa mizito. 53 Hata walipokwisha kuvuka, walifika nchi ya Genesareti, wakatia nanga. 54 Nao wakiisha kutoka mashuani, mara watu walimtambua, 55 wakaenda mbio, wakizunguka nchi ile yote, wakaanza kuwachukua vitandani walio hawawezi, kwenda kila mahali waliposikia kwamba yupo. 56 Na kila alikokwenda, akiingia vijijini, au mijini, au mashambani, wakawaweka wagonjwa sokoni, wakamsihi waguse ngaa pindo la vazi lake; nao wote waliomgusa wakapona.

Marko 7

1 Kisha Mafarisayo, na baadhi ya waandishi waliotoka Yerusalemu, wakakusanyika mbele yake, 2 wakaona wengine katika wanafunzi wake wakila vyakula kwa mikono najisi, yaani, isiyonawiwa. 3 Kwa maana Mafarisayo na Wayahudi wote wasiponawa mikono mpaka kiwiko, hawali, wakishika mapokeo ya wazee wao; 4 tena wakitoka sokoni, wasipotawadha, hawali; na yako mambo mengine waliyopokea kuyashika, kama kuosha vikombe, na midumu, na vyombo vya shaba. 5 Basi wale Mafarisayo na waandishi wakamwuliza, Mbona wanafunzi wako hawaendi kwa kuyafuata mapokeo ya wazee, bali hula chakula kwa mikono najisi? 6 Akawaambia, Isaya alitabiri vema juu yenu ninyi wanafiki, kama ilivyoandikwa, Watu hawa huniheshimu kwa midomo Ila mioyo yao iko mbali nami; 7 Nao waniabudu bure, Wakifundisha mafundisho Yaliyo maagizo ya wanadamu, 8 Ninyi mwaiacha amri ya Mungu, na kuyashika mapokeo ya wanadamu. 9 Akawaambia, Vema! Mwaikataa amri ya Mungu mpate kuyashika mapokeo yenu. 10 Maana Musa alisema, Waheshimu baba yako na mama yako, na, Amtukanaye babaye au mamaye kufa na afe. 11 Bali ninyi husema, Mtu akimwambia babaye au mamaye, Ni Korbani, yaani, wakfu, kitu changu cho chote kikupasacho kufaidiwa nacho, huwa basi; 12 wala hammruhusu baada ya hayo kumtendea neno babaye au mamaye; 13 huku mkilitangua neno la Mungu kwa mapokeo yenu mliyopokeana; tena mwafanya mambo mengi yaliyo sawasawa na hayo. 14 Akawaita makutano tena, akawaambia, Nisikieni nyote na kufahamu. 15 Hakuna kitu kilicho nje ya mtu ambacho kikimwingia chaweza kumtia unajisi, bali vile vimtokavyo, ndivyo vimtiavyo unajisi yule mtu. 16 Mtu akiwa na masikio ya kusikilia, na asikie. 17 Hata alipoingia nyumbani, ameuacha mkutano, wanafunzi wake wakamwuliza habari za ule mfano. 18 Akawaambia, Hivi hata ninyi hamna akili? Hamfahamu ya kwamba kila kitu kilicho nje ya mtu, kikimwingia, hakiwezi kumtia unajisi; 19 kwa sababu hakimwingii moyoni, ila tumboni tu; kisha chatoka kwenda chooni? Kwa kusema hivi alivitakasa vyakula vyote. 20 Akasema, Kimtokacho mtu ndicho kimtiacho unajisi. 21 Kwa maana ndani ya mioyo ya watu hutoka mawazo mabaya, uasherati, 22 wivi, uuaji, uzinzi, tamaa mbaya, ukorofi, hila, ufisadi, kijicho, matukano, kiburi, upumbavu. 23 Haya yote yaliyo maovu yatoka ndani, nayo yamtia mtu unajisi. 24 Akaondoka huko, akaenda zake hata mipaka ya Tiro na Sidoni. Akaingia katika nyumba, akataka isijulikane na mtu; lakini hakuweza kusitirika. 25 Ila mara mwanamke, ambaye binti yake yuna pepo mchafu, alisikia habari zake, akaja akamwangukia miguuni pake. 26 Na yule mwanamke ni Myunani, kabila yake ni Msirofoinike. Akamwomba amtoe pepo katika binti yake. 27 Akamwambia, Waache watoto washibe kwanza; maana si vizuri kukitwaa chakula cha watoto, na kuwatupia mbwa. 28 Naye akajibu, akamwambia, Naam, Bwana, lakini hata mbwa walio chini ya meza hula makombo ya watoto. 29 Akamwambia, Kwa sababu ya neno hilo, enenda zako, pepo amemtoka binti yako. 30 Akaenda zake nyumbani kwake, akamkuta yule kijana amelazwa kitandani, na yule pepo amekwisha kumtoka. 31 Akatoka tena katika mipaka ya Tiro, akapita katikati ya Sidoni, akaenda mpaka bahari ya Galilaya, kati ya mipaka ya Dekapoli. 32 Wakamletea kiziwi, naye ni mwenye utasi, wakamsihi amwekee mikono. 33 Akamtenga na mkutano faraghani, akatia vidole vyake masikioni mwake, akatema mate, akamgusa ulimi, 34 akatazama juu mbinguni, akaugua, akamwambia, Efatha, maana yake, Funguka. 35 Mara masikio yake yakafunguka, kifungo cha ulimi wake kikalegea, akasema vizuri. 36 Akawaonya wasimwambie mtu; lakini kadiri ya alivyozidi kuwaagiza, ndivyo walivyozidi kutangaza habari; 37 wakashangaa mno kupita kiasi, wakinena, Ametenda mambo yote vema; viziwi awafanya wasikie, na bubu waseme.

Marko 8

1 Katika siku zile, kwa vile ulivyokuwa mkuu tena ule mkutano, nao wamekosa kitu cha kula, akawaita wanafunzi wake, akawaambia, 2 Nawahurumia mkutano kwa sababu yapata siku tatu wamekaa nami, wala hawana kitu cha kula; 3 nami nikiwaaga waende zao nyumbani kwao hali wanafunga, watazimia njiani; na baadhi yao wametoka mbali. 4 Wanafunzi wake wakamjibu, Je! Ataweza wapi mtu kuwashibisha hawa mikate hapa nyikani? 5 Akawauliza, Mnayo mikate mingapi? Wakasema, Saba, 6 Akawaagiza mkutano waketi chini; akaitwaa ile mikate saba, akashukuru, akaimega, akawapa wanafunzi wake wawaandikie; wakawaandikia mkutano. 7 Walikuwa na visamaki vichache; akavibarikia, akasema wawaandikie na hivyo pia. 8 Wakala, wakashiba, wakakusanya mabaki ya vipande vya mikate makanda saba. 9 Na watu waliokula wapata elfu nne. Akawaaga. 10 Mara akapanda chomboni pamoja na wanafunzi wake, akaenda pande za Dalmanutha. 11 Wakatokea Mafarisayo, wakaanza kuhojiana naye; wakitafuta kwake ishara itokayo mbinguni; wakimjaribu. 12 Akaugua rohoni mwake, akasema, Mbona kizazi hiki chatafuta ishara? Amin, nawaambieni, Hakitapewa ishara kizazi hiki. 13 Akawaacha, akapanda tena chomboni, akaenda zake hata ng'ambo. 14 Wakasahau kuchukua mikate, wala chomboni hawana ila mkate mmoja tu. 15 Akawaagiza, akasema, Angalieni, jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode. 16 Wakabishana wao kwa wao, kwa kuwa hawana mikate. 17 Naye Yesu akatambua, akawaambia, Mbona mnabishana kwa sababu hamna mikate? Hamfahamu bado, wala hamjaelewa? Je! Mioyo yenu ni mizito? 18 Mna macho, hamwoni; mna masikio, hamsikii? Wala hamkumbuki? 19 Nilipoivunja ile mikate mitano na kuwapa wale elfu tano, mlichukua vikapu vingapi vimejaa vipande? Wakamwambia, Kumi na viwili. 20 Na ile saba kuwapa wale elfu nne, mlichukua makanda mangapi yamejaa vipande? Wakamwambia, Saba. 21 Akawaambia, Hamjafahamu bado? 22 Wakafika Bethsaida, wakamletea kipofu, wakamsihi amguse. 23 Akamshika mkono yule kipofu, akamchukua nje ya kijiji, akamtemea mate ya macho, akamwekea mikono yake, akamwuliza, Waona kitu? 24 Akatazama juu, akasema, Naona watu kama miti, inakwenda. 25 Ndipo akaweka tena mikono yake juu ya macho yake, naye akatazama sana; akawa mzima, akaona vyote waziwazi. 26 Akampeleka nyumbani kwake, akisema, Hata kijijini usiingie. 27 Akatoka Yesu na wanafunzi wake, wakaenda kwenye vijiji vya Kaisaria-Filipi; na njiani akawauliza wanafunzi wake, akasema, Watu huninena mimi kuwa ni nani? 28 Wakamjibu, Yohana Mbatizaji; wengine, Eliya; wengine, Mmojawapo wa manabii. 29 Naye akawauliza, Na ninyi mnasema ya kuwa mimi ni nani? Petro akamjibu, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo. 30 Akawaonya wasimwambie mtu habari zake. 31 Akaanza kuwafundisha kwamba imempasa Mwana wa Adamu kupatikana na mateso mengi, na kukataliwa na wazee, na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na baada ya siku tatu kufufuka. 32 Naye alikuwa akinena neno hilo waziwazi. Petro akamchukua, akaanza kumkemea. 33 Akageuka, akawatazama wanafunzi wake, akamkemea Petro, akasema, Nenda nyuma yangu, Shetani; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu. 34 Akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, Mtu ye yote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate. 35 Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha. 36 Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? 37 Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake? 38 Maana kila mtu atakayenionea haya mimi, na maneno yangu, katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.

Marko 9

1 Akawaambia, Amin, nawaambia, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapouona ufalme wa Mungu umekuja kwa nguvu. 2 Hata baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani, peke yao; akageuka sura yake mbele yao; 3 mavazi yake yakimeta-meta, meupe mno, jinsi asivyoweza dobi duniani kuyafanya meupe. 4 Wakatokewa na Eliya pamoja na Musa, nao walikuwa wakizungumza na Yesu. 5 Petro akajibu, akamwambia Yesu, Rabi, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu, kimoja chako wewe, kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. 6 Maana, hakujua la kunena, kwa kuwa waliingiwa na hofu nyingi. 7 Kisha likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye. 8 Mara hiyo walipotazama huku na huku, hawakuona mtu pamoja nao ila Yesu peke yake. 9 Na walipokuwa wakishuka mlimani aliwakataza wasimweleze mtu waliyoyaona, hata Mwana wa Adamu atakapokuwa amefufuka katika wafu. 10 Wakalishika neno lile, wakiulizana wao kwa wao, Huko kufufuka katika wafu maana yake nini? 11 Wakamwuliza, wakisema, Mbona waandishi hunena ya kwamba imempasa Eliya kuja kwanza? 12 Akajibu akawaambia, Ni kweli Eliya yuaja kwanza, na kurejeza upya yote; lakini, pamoja na haya, ameandikiwaje Mwana wa Adamu ya kwamba atateswa mengi na kudharauliwa? 13 Lakini nawaambia, Eliya amekwisha kuja, nao wakamtenda yote waliyoyataka kama alivyoandikiwa. 14 Hata walipowafikia wanafunzi, waliona mkutano mkuu wakiwazunguka, na waandishi wakijadiliana nao; 15 mara mkutano wote walipomwona walishangaa, wakamwendea mbio, wakamsalimu. 16 Akawauliza, Mnajadiliana nini nao? 17 Mtu mmoja katika mkutano akamjibu, Mwalimu, nimemleta mwanangu kwako, ana pepo bubu; 18 na kila ampagaapo, humbwaga chini, naye hutoka povu na kusaga meno na kukonda; nikasema na wanafunzi wako wamtoe pepo, wasiweze. 19 Akawajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni kwangu. 20 Wakamleta kwake; hata alipomwona, mara yule pepo alimtia kifafa; naye akaanguka chini, akagaa-gaa, akitokwa na povu. 21 Akamwuliza babaye, Amepatwa na haya tangu lini? Akasema, Tangu utoto. 22 Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia. 23 Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye. 24 Mara babaye yule kijana akapaza sauti, akasema, Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu. 25 Naye Yesu akiona ya kuwa mkutano unakusanyika mbio, akamkemea yule pepo mchafu, akamwambia, Ewe pepo bubu na kiziwi, mimi nakuamuru, mtoke huyu, wala usimwingie tena. 26 Akalia, akamtia kifafa sana, akamtoka; naye akawa kama amekufa; hata wengi wakasema, Amekufa. 27 Lakini Yesu akamshika mkono akamwinua naye akasimama. 28 Hata alipoingia nyumbani, wanafunzi wake wakamwuliza kwa faragha, Mbona sisi hatukuweza kumtoa? 29 Akawaambia, Namna hii haiwezi kutoka kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba. 30 Wakatoka huko, wakapita katikati ya Galilaya; naye hakutaka mtu kujua. 31 Kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka. 32 Lakini hawakulifahamu neno lile, wakaogopa kumwuliza. 33 Wakafika Kapernaumu; hata alipokuwamo nyumbani, akawauliza, Mlishindania nini njiani? 34 Wakanyamaza; kwa maana njiani walikuwa wakibishana wao kwa wao, ni nani aliye mkubwa. 35 Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote. 36 Akatwaa kitoto, akamweka katikati yao, akamkumbatia, akawaambia, 37 Mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi; na mtu akinipokea mimi, humpokea, si mimi, bali yeye aliyenituma. 38 Yohana akamjibu, akamwambia, Mwalimu, tulimwona mtu akitoa pepo kwa jina lako, ambaye hafuatani nasi; tukamkataza, kwa sababu hafuatani nasi. 39 Yesu akasema, Msimkataze, kwa kuwa hakuna mtu atakayefanya mwujiza kwa jina langu akaweza mara kuninenea mabaya; 40 kwa sababu asiye kinyume chetu, yu upande wetu. 41 Kwa kuwa ye yote atakayewanywesha ninyi kikombe cha maji, kwa kuwa ninyi ni watu wa Kristo, amin, nawaambia, hatakosa thawabu yake. 42 Na ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini. 43 Na mkono wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima u kigutu, kuliko kuwa na mikono miwili, na kwenda zako jehanum, kwenye moto usiozimika; 44 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki. 45 Na mguu wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima, u kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili, na kutupwa katika jehanum; 46 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki. 47 Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum; 48 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki. 49 Kwa sababu kila mtu atatiwa chumvi kwa moto. 50 Chumvi ni njema; lakini chumvi ikiwa si chumvi tena, mtaitia nini ikolee? Mwe na chumvi ndani yenu, mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi.

Marko 10

1 Akaondoka huko akafika mipakani mwa Uyahudi, na ng'ambo ya Yordani; makutano mengi wakakutanika tena wakamwendea; akawafundisha tena kama alivyozoea. 2 Basi Mafarisayo wakamwendea, wakamwuliza, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe? Huku wakimjaribu. 3 Naye akajibu, akawaambia, Musa aliwaamuru nini? 4 Wakasema, Musa alitoa ruhusa kuandika hati ya talaka na kumwacha. 5 Yesu akawaambia, Kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu aliwaandikia amri hii. 6 Lakini tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke. 7 Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; 8 na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. 9 Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe. 10 Hata nyumbani tena wanafunzi wakamwuliza habari ya neno hilo. 11 Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; 12 na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini. 13 Basi wakamletea watoto wadogo ili awaguse; wanafunzi wake wakawakemea. 14 Ila Yesu alipoona alichukizwa sana, akawaambia, Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie; kwa maana watoto kama hawa ufalme wa Mungu ni wao. 15 Amin, nawaambieni, Ye yote asiyeukubali ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hatauingia kabisa. 16 Akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao, akawabarikia. 17 Hata alipokuwa akitoka kwenda njiani, mtu mmoja akaja mbio, akampigia magoti, akamwuliza, Mwalimu mwema, nifanye nini nipate kuurithi uzima wa milele? 18 Yesu akamwambia, Kwa nini kuniita mwema? Hakuna aliye mwema ila mmoja, ndiye Mungu. 19 Wazijua amri, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, Usidanganye, Waheshimu baba yako na mama yako. 20 Akamwambia, Mwalimu, haya yote nimeyashika tangu utoto wangu. 21 Yesu akamkazia macho, akampenda, akamwambia, Umepungukiwa na neno moja. Enenda, ukauze ulivyo navyo vyote, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate. 22 Walakini yeye akakunja uso kwa neno hilo, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi. 23 Yesu akatazama kotekote, akawaambia wanafunzi wake, Jinsi itakavyokuwa shida wenye mali kuingia katika ufalme wa Mungu! 24 Wanafunzi wakashangaa kwa maneno yake. Yesu akajibu tena, akawaambia, Watoto, jinsi ilivyo shida wenye kutegemea mali kuingia katika ufalme wa Mungu! 25 Ni rahisi ngamia kupenya katika tundu ya sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu. 26 Nao wakashangaa mno, wakimwambia, Ni nani, basi, awezaye kuokoka? 27 Yesu akawakazia macho, akasema, Kwa wanadamu haiwezekani, bali kwa Mungu sivyo; maana yote yawezekana kwa Mungu. 28 Petro akaanza kumwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe. 29 Yesu akasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, 30 ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele. 31 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho; na wa mwisho watakuwa wa kwanza. 32 Nao walikuwako njiani, huku wakipanda kwenda Yerusalemu; na Yesu alikuwa akiwatangulia, wakashangaa, nao katika kufuata wakaogopa. Akawatwaa tena wale Thenashara, akaanza kuwaambia habari za mambo yatakayompata, 33 akisema, Angalieni, tunapanda kwenda Yerusalemu; na Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi, nao watamhukumu afe, watamtia mikononi mwa Mataifa, 34 nao watamdhihaki, na kumtemea mate, na kumpiga mijeledi, na kumwua; na baada ya siku tatu atafufuka. 35 Na Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, wakamwendea, wakamwambia, Mwalimu, twataka utufanyie lo lote tutakalokuomba. 36 Akawaambia, Mwataka niwafanyie nini? 37 Wakamwambia, Utujalie sisi tuketi, mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika utukufu wako. 38 Yesu akawaambia, Hamjui mnaloliomba. Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi? 39 Wakamwambia, Twaweza. Yesu akawaambia, Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; 40 lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari. 41 Hata wale kumi waliposikia wakaanza kuwakasirikia Yakobo na Yohana. 42 Yesu akawaita, akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. 43 Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, 44 na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote. 45 Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi. 46 Wakafika Yeriko; hata alipokuwa akishika njia kutoka Yeriko, pamoja na wanafunzi wake, na mkutano mkubwa, mwana wa Timayo, Bartimayo, yule mwombaji kipofu, alikuwa ameketi kando ya njia. 47 Naye aliposikia ya kwamba ni Yesu Mnazareti, alianza kupaza sauti yake, na kusema, Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu. 48 Na wengi wakamkemea ili anyamaze, lakini alizidi kupaza sauti, Mwana wa Daudi, unirehemu. 49 Yesu akasimama akasema, Mwiteni. Wakamwita yule kipofu, wakamwambia, Jipe moyo; inuka, anakuita. 50 Akatupa vazi lake, akaruka, akamwendea Yesu. 51 Yesu akamjibu, akamwambia, Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona. 52 Yesu akamwambia, Enenda zako, imani yako imekuponya. Mara akapata kuona; akamfuata njiani.

Marko 11

1 Hata walipokaribia Yerusalemu karibu na Bethfage na Bethania, kukabili mlima wa Mizeituni, aliwatuma wawili katika wanafunzi wake, 2 akawaambia, Nendeni mpaka kile kijiji kinachowakabili; na katika kuingia ndani yake, mara mtaona mwana-punda amefungwa, asiyepandwa na mtu bado; mfungueni, kamleteni. 3 Na mtu akiwaambia, Mbona mnafanya hivi? Semeni, Bwana anamhitaji na mara atamrudisha tena hapa. 4 Wakaenda zao, wakamwona mwana-punda amefungwa penye mlango, nje katika njia kuu, wakamfungua. 5 Baadhi ya watu waliosimama huko wakawaambia, Mnafanya nini kumfungua mwana-punda? 6 Wakawaambia kama Yesu alivyowaagiza, nao wakawaruhusu. 7 Wakamletea Yesu yule mwana-punda, wakatandika mavazi yao juu yake; akaketi juu yake. 8 Watu wengi wakatandaza mavazi yao njiani, na wengine matawi waliyoyakata mashambani. 9 Nao watu waliotangulia na wale waliofuata wakapaza sauti, Hosana; ndiye mbarikiwa ajaye kwa jina la Bwana; 10 umebarikiwa na ufalme ujao, wa baba yetu Daudi. Hosana juu mbinguni. 11 Naye akaingia Yerusalemu hata ndani ya hekalu; na alipokwisha kutazama yote pande zote, kwa kuwa ni wakati wa jioni, akatoka, akaenda Bethania pamoja na wale Thenashara. 12 Hata asubuhi yake walipotoka Bethania aliona njaa. 13 Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda aone kitu juu yake; na alipoufikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati wa tini. 14 Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako. Wanafunzi wake wakasikia. 15 Wakafika Yerusalemu, naye akaingia ndani ya hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza na kununua ndani ya hekalu, akazipindua meza za wabadili fedha, na viti vyao wauzao njiwa; 16 wala hakuacha mtu achukue chombo kati ya hekalu. 17 Akafundisha, akasema, Je! Haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi. 18 Wakuu wa makuhani na waandishi wakapata habari wakatafuta jinsi ya kumwangamiza; maana walimwogopa, kwa sababu mkutano wote walishangaa kwa mafundisho yake. 19 Na kulipokuwa jioni alitoka mjini. 20 Na asubuhi walipokuwa wakipita, waliuona ule mtini umenyauka toka shinani. 21 Petro akakumbuka habari yake, akamwambia, Rabi, tazama, mtini ulioulaani umenyauka. 22 Yesu akajibu, akamwambia, Mwaminini Mungu. 23 Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng'oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. 24 Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu. 25 Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. 26 Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu. 27 Wakafika Yerusalemu tena; hata alipokuwa akitembea hekaluni, walimwendea wakuu wa makuhani, na waandishi, na wazee, 28 wakamwambia, Ni kwa mamlaka gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa mamlaka hii uyatende haya? 29 Yesu akawaambia, Nitawauliza neno moja, nanyi mnijibu, kisha nitawaambia ni kwa mamlaka gani nayatenda haya. 30 Ubatizo wa Yohana ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu? Nijibuni. 31 Wakasemezana wao kwa wao, wakisema, Kama tukisema, Ulitoka mbinguni, atasema, Mbona, basi, hamkumwamini? 32 Ila tukisema, Ulitoka kwa wanadamu, -- waliogopa watu; maana watu wote walimwona Yohana kuwa nabii halisi. 33 Wakamjibu Yesu, wakasema, Hatujui. Yesu akawaambia, Wala mimi siwaambii ninyi ni kwa mamlaka gani nayatenda haya.

Marko 12

1 Akaanza kusema nao kwa mifano; Mtu mmoja alipanda shamba la mizabibu, akazungusha ugo, akachimba shimo la shinikizo, akajenga mnara, akapangisha wakulima, akasafiri. 2 Hata kwa wakati wake akatuma mtumwa kwa wale wakulima, ili apokee kwa wakulima katika matunda ya mizabibu. 3 Wakamtwaa, wakampiga, wakamtoa nje, hana kitu. 4 Akatuma tena kwao mtumwa mwingine, na huyo wakamtia jeraha za kichwa, wakamfanyia jeuri. 5 Akamtuma mwingine, huyo wakamwua; na wengine wengi, hawa wakiwapiga na hawa wakiwaua. 6 Basi alikuwa na mmoja bado, mwana mpendwa wake; huyu naye akamtuma kwao mwisho, akisema, Watamstahi mwanangu. 7 Lakini wale wakulima wakasemezana, Huyu ni mrithi; haya, na tumwue, na urithi utakuwa wetu. 8 Wakamkamata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu. 9 basi atafanyaje yule bwana wa shamba la mizabibu? Atakuja na kuwaangamiza wale wakulima, na lile shamba la mizabibu atawapa wengine. 10 Hata andiko hili hamjalisoma, Jiwe walilolikataa waashi, Hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni. 11 Neno hili limetoka kwa Bwana, Nalo ni ajabu machoni petu? 12 Nao wakatafuta kumkamata, wakaogopa mkutano; maana walitambua ya kwamba ule mfano amewanenea wao. Wakamwacha wakaenda zao. 13 Wakatuma kwake baadhi ya Mafarisayo na Maherodi, ili wamnase kwa maneno. 14 Hata walipofika walimwambia, Mwalimu, twajua ya kuwa wewe u mtu wa kweli, wala hujali cheo cha mtu; kwa maana hutazami sura za watu; lakini katika kweli waifundisha njia ya Mungu. Je! Ni halali kumpa Kaisari kodi au siyo? 15 Tumpe, tusimpe? Naye, akijua unafiki wao, akawaambia, Mbona mmenijaribu? Nileteeni dinari niione. 16 Wakaileta. Akawaambia, Ni ya nani sanamu hii na anwani hii? Wakamwambia, Ni ya Kaisari. 17 Yesu akajibu, akawaambia, Mpeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na yaliyo ya Mungu mpeni Mungu. Wakamstaajabia sana. 18 Kisha Masadukayo, watu wasemao ya kwamba hakuna kiyama, wakamwendea, wakamwuliza na kusema, 19 Mwalimu, Musa alituandikia ya kwamba ndugu ya mtu akifa, akamwacha mkewe wala hana mtoto, ndugu yake amtwae yule mkewe akampatie ndugu yake mzao. 20 Basi kulikuwa na ndugu saba, wa kwanza akatwaa mke, akafa, asiache mzao. 21 Wa pili naye akamtwaa akafa, wala yeye hakuacha mzao. Na wa tatu kadhalika; 22 hata na wote saba, wasiache mzao. Mwisho wa wote yule mwanamke akafa naye. 23 Basi, katika kiyama atakuwa mke wa yupi katika hao? Maana wote saba walikuwa naye. 24 Yesu akajibu, akawaambia, Je! Hampotei kwa sababu hii, kwa kuwa hamyajui maandiko wala uweza wa Mungu? 25 Kwa maana watakapofufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika walioko mbinguni. 26 Na kwa habari ya wafu ya kwamba wafufuliwa, hamjasoma katika kitabu cha Musa, Sura ya Kijiti, jinsi Mungu alivyomwambia, akisema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? 27 Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Hivyo mwapotea sana. 28 Na mmojawapo wa waandishi akafika, akawasikia wakisemezana naye, akatambua ya kuwa amewajibu vema, akamwuliza, Katika amri zote ni ipi iliyo ya kwanza? 29 Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; 30 nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote. 31 Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi. 32 Yule mwandishi akamwambia, Hakika, Mwalimu, umesema vema ya kwamba Mungu ni mmoja, wala hakuna mwingine ila yeye; 33 na kumpenda yeye kwa moyo wote, na kwa ufahamu wote, na kwa nguvu zote, na kumpenda jirani kama nafsi yako, kwafaa kuliko sadaka nzima za kuteketezwa na dhahibu zote pia. 34 Naye Yesu, alipoona kwamba amejibu kwa busara, alimwambia, Wewe hu mbali na ufalme wa Mungu. Wala hakuthubutu mtu kumsaili neno tena tokea hapo. 35 Hata Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu, alijibu, akasema, Husemaje waandishi ya kwamba Kristo ni Mwana wa Daudi? 36 Daudi mwenyewe alisema, kwa uweza wa Roho Mtakatifu, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwawekapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako. 37 Daudi mwenyewe asema ni Bwana; basi amekuwaje mwanawe? Na mkutano mkubwa walikuwa wakimsikiliza kwa furaha. 38 Akawaambia katika mafundisho yake, Jihadharini na waandishi, wapendao kutembea wamevaa mavazi marefu, na kusalimiwa masokoni, 39 na kuketi mbele katika masinagogi, na viti vya mbele katika karamu; 40 ambao hula nyumba za wajane, na kwa unafiki husali sala ndefu; hawa watapata hukumu iliyo kubwa. 41 Naye akaketi kulielekea sanduku la hazina, akatazama jinsi mkutano watiavyo mapesa katika sanduku. Matajiri wengi wakatia mengi. 42 Akaja mwanamke mmoja, mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu pesa. 43 Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina; 44 maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia.

Marko 13

1 Hata alipokuwa akitoka hekaluni, mmoja wa wanafunzi wake alimwambia, Mwalimu, tazama, yalivyo mawe na majengo haya! 2 Yesu akajibu, akamwambia, Wayaona majengo haya makubwa? Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomolewa. 3 Hata alipokuwa ameketi katika mlima wa Mizeituni, kuelekea hekalu Petro, na Yakobo, na Yohana, na Andrea walimwuliza kwa faragha, 4 Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya wakati, hayo yote yatakapokuwa karibu kutimia? 5 Yesu akaanza kuwaambia, Jihadharini, mtu asiwadanganye. 6 Wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ndiye, nao watadanganya wengi. 7 Nanyi mtakaposikia habari za vita na uvumi wa vita, msitishwe; hayo hayana budi kutukia, lakini ule mwisho bado. 8 Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko ya nchi mahali mahali; kutakuwako na njaa; hayo ndiyo mwanzo wa utungu. 9 Nanyi jihadharini nafsi zenu; maana watawapeleka ninyi mabarazani; na katika masinagogi mtapigwa; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao. 10 Na sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote. 11 Na watakapowachukua ninyi, na kuwasaliti, msitafakari kwanza mtakayosema, lakini lo lote mtakalopewa saa ile, lisemeni; kwa maana si ninyi msemao, bali ni Roho Mtakatifu. 12 Na ndugu atamsaliti ndugu yake ili auawe, na baba atamsaliti mtoto, na watoto watashambulia wazazi wao, na kuwafisha. 13 Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kusaburi hata mwisho, ndiye atakayeokoka. 14 Lakini mlionapo chukizo la uharibifu likisimama pasipolipasa, (asomaye na afahamu), ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani; 15 na mtu aliye juu ya dari asishuke, wala asiingie kuchukua kitu nyumbani mwake; 16 naye aliye shambani asirudi nyuma kulichukua vazi lake. 17 Lakini ole wao wenye mimba, nao wanyonyeshao siku hizo! 18 Ila ombeni yasitokee hayo wakati wa baridi. 19 Kwa maana siku hizo zitakuwa na dhiki, jinsi isivyokuwa tangu mwanzo wa kuumba alipoumba Mungu hata sasa, wala haitakuwa kamwe. 20 Na kama Bwana asingalizikatiza siku hizo, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule aliowateua amezikatiza siku hizo. 21 Na wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule, msisadiki; 22 kwa maana wataondoka Makristo wa uongo, na manabii wa uongo, watatoa ishara na maajabu, wapate kuwadanganya, kama yamkini, hata hao wateule. 23 Bali ninyi jihadharini; nimekwisha kuwaonya yote mbele. 24 Lakini siku zile, baada ya dhiki hiyo, jua litatiwa giza, na mwezi hatautoa mwanga wake. 25 na nyota za mbinguni zitakuwa zikianguka, na nguvu zilizo mbinguni zitatikisika. 26 Hapo ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija mawinguni kwa nguvu nyingi na utukufu. 27 Ndipo atakapowatuma malaika na kuwakusanya wateule wake toka pepo nne, toka upande wa mwisho wa nchi hata upande wa mwisho wa mbingu. 28 Kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake liishapo kuwa laini, na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno ni karibu; 29 nanyi kadhalika, myaonapo mambo hayo yanaanza, tambueni ya kuwa yu karibu milangoni. 30 Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatimie. 31 Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe. 32 Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba. 33 Angalieni, kesheni, ombeni, kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo. 34 Mfano wake ni kama mtu mwenye kusafiri, ameiacha nyumba yake, amewapa watumwa wake amri, na kila mtu kazi yake, naye amemwamuru bawabu akeshe. 35 Kesheni basi, kwa maana hamjui ajapo bwana wa nyumba, kwamba ni jioni, au kwamba ni usiku wa manane, au awikapo jimbi, au asubuhi; 36 asije akawasili ghafula akawakuta mmelala. 37 Na hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.

Marko 14

1 Baada ya siku mbili ilikuwa sikukuu ya Pasaka, na mikate isiyochachwa; wakuu wa makuhani na waandishi wakatafuta njia ya kumkamata kwa hila na kumwua. 2 Kwa maana walisema, Isiwe kwa wakati wa sikukuu, isije ikatokea ghasia katika watu. 3 Naye alipokuwapo Bethania, nyumbani mwa Simoni mkoma, ameketi chakulani, alikuja mwanamke mwenye kibweta cha marhamu ya nardo safi ya thamani nyingi; akakivunja kibweta akaimimina kichwani pake. 4 Palikuwa na watu waliochukizwa katika nafsi zao wakisema, Kwani kupoteza marhamu namna hii? 5 Maana marhamu hii ingaliweza kuuzwa kwa dinari mia tatu na kuzidi, wakapewa maskini. Wakamnung'unikia sana yule mwanamke. 6 Yesu akasema, Mwacheni; mbona mnamtaabisha? Amenitendea kazi njema; 7 maana sikuzote mnao maskini pamoja nanyi, na kila mpendapo mwaweza kuwatendea mema; lakini mimi hamnami sikuzote. 8 Ametenda alivyoweza; ametangulia kuupaka mwili wangu marhamu kwa ajili ya maziko. 9 Amin, nawaambia, Kila ihubiriwapo Injili katika ulimwengu wote, na hili alilotenda huyu litatajwa kwa kumbukumbu lake. 10 Yuda Iskariote, yule mmoja katika wale Thenashara, akaenda zake kwa wakuu wa makuhani, apate kumsaliti kwao. 11 Nao waliposikia walifurahi, wakaahidi kumpa fedha. Akatafuta njia ya kumsaliti wakati wa kufaa. 12 Hata siku ya kwanza ya mikate isiyochachwa, walipoichinja pasaka, wanafunzi wake wakamwambia, Ni wapi utakapo tuende tukuandalie uile pasaka? 13 Akatuma wawili katika wanafunzi wake, akawaambia, Nendeni zenu mjini; atakutana nanyi mwanamume amechukua mtungi wa maji; mfuateni; 14 na po pote atakapoingia, mwambieni mwenye nyumba, Mwalimu asema, Ki wapi chumba changu cha wageni, niile pasaka humo, pamoja na wanafunzi wangu? 15 Naye mwenyewe atawaonyesha orofa kubwa, imeandikwa tayari; humo tuandalieni. 16 Wanafunzi wakatoka, wakaenda mjini, wakaona kama alivyowaambia, wakaiandaa pasaka. 17 Basi ilipokuwa jioni yuaja pamoja na wale Thenashara. 18 Nao walipokuwa wameketi chakulani, wakila, Yesu alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu, naye anakula pamoja nami, atanisaliti. 19 Wakaanza kuhuzunika, wakamwambia mmoja mmoja, Je! Ni mimi? 20 Akawaambia, Ni mmoja wa hao Thenashara, ambaye achovya pamoja nami katika kombe. 21 Kwa maana Mwana wa Adamu aenda zake kama alivyoandikiwa; lakini ole wake mtu yule ambaye amsaliti Mwana wa Adamu; ingekuwa heri kwake mtu yule kama asingalizaliwa. 22 Nao walipokuwa wakila, alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa, akasema, Twaeni; huu ndio mwili wangu. 23 Akatwaa kikombe, akashukuru, akawapa; wakakinywea wote. 24 Akawaambia, Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi. 25 Amin, nawaambia ninyi, Sitakunywa tena kabisa uzao wa mzabibu, hata siku ile nitakapounywa mpya katika ufalme wa Mungu. 26 Nao walipokwisha kuimba walitoka kwenda mlima wa Mizeituni. 27 Yesu akawaambia, Mtakunguwazwa ninyi nyote kwa ajili yangu usiku huu; kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo watatawanyika. 28 Lakini baada ya kufufuka kwangu, nitawatangulia kwenda Galilaya. 29 Petro akamwambia, Hata wajapokunguwazwa wote, lakini siyo mimi. 30 Yesu akamwambia, Amin, nakuambia wewe, Leo, usiku huu, kabla ya kuwika jogoo mara mbili, utanikana mara tatu. 31 Naye akazidi sana kusema, Ijaponipasa kufa nawe, hata hivyo sitakukana kamwe. Na wote wakasema vile vile. 32 Kisha wakaja mpaka bustani iitwayo Gethsemane; akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa muda niombapo. 33 Akamtwaa Petro na Yakobo na Yohana pamoja naye, akaanza kufadhaika sana na kuhangaika. 34 Akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa mkeshe. 35 Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifudifudi, akiomba ya kuwa, ikiwezekana, saa hiyo imwepuke. 36 Akasema, Aba, Baba, yote yawezekana kwako; uniondolee kikombe hiki; walakini, si kama nitakavyo mimi, bali utakavyo wewe. 37 Akaja akawakuta wamelala usingizi, akamwambia Petro, Je! Simoni, umelala? Hukuweza kukesha saa moja? 38 Kesheni mwombe, msije mkaingia majaribuni, roho i radhi ila mwili ni dhaifu. 39 Akaenda zake tena, akaomba, akisema neno lilo hilo. 40 Akaja tena akawakuta wamelala, maana macho yao yamekuwa mazito, wala hawakujua la kumjibu. 41 Akaja mara ya tatu, akawaambia, Laleni sasa, mpumzike; yatosha, saa imekuja; tazama, Mwana wa Adamu anatiwa mikononi mwao wenye dhambi. 42 Ondokeni, twendeni zetu; tazama, yule anayenisaliti amekaribia. 43 Basi alipokuwa katika kusema, mara Yuda alifika, mmoja wa wale Thenashara, na pamoja naye mkutano, wana panga na marungu, wametoka kwa wakuu wa makuhani, na waandishi, na wazee. 44 Na yule anayemsaliti alikuwa amewapa ishara, akisema, Nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni, mkamchukue salama. 45 Basi alipokuja, mara akamwendea, akasema, Rabi, akambusu. 46 Wakanyosha mikono yao wakamkamata. 47 Na mmoja wao waliokuwapo akafuta upanga, akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio. 48 Yesu akajibu, akawaambia, Je! Ni kama juu ya mnyang'anyi mmetoka wenye panga na marungu, kunitwaa mimi? 49 Kila siku nalikuwa mbele yenu hekaluni nikifundisha, msinikamate; lakini haya yamekuwa ili maandiko yapate kutimia. 50 Ndipo wakamwacha, wakakimbia wote. 51 Na kijana mmoja alimfuata, amejitanda mwili wake nguo ya kitani; wakamkamata; 52 naye akaiacha ile nguo ya kitani, akakimbia yu uchi. 53 Nao wakamchukua Yesu kwa Kuhani Mkuu; wakamkusanyikia wote, wakuu wa makuhani na wazee na waandishi. 54 Naye Petro akamfuata kwa mbali, hata ndani katika behewa ya Kuhani Mkuu; akawa ameketi pamoja na watumishi, anakota moto mwangani. 55 Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda juu ya Yesu wapate kumwua; wasione. 56 Kwa maana wengi walimshuhudia uongo, walakini ushuhuda wao haukupatana. 57 Hata wengine wakasimama, wakamshuhudia uongo, wakisema, 58 Sisi tulimsikia akisema, Mimi nitalivunja hekalu hili lililofanyika kwa mikono, na katika siku tatu nitajenga jingine lisilofanyika kwa mikono. 59 Wala hata hivi ushuhuda wao haukupatana. 60 Kisha Kuhani Mkuu akasimama katikati, akamwuliza Yesu, akisema, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? 61 Lakini akanyamaza, wala hakujibu neno. Kuhani Mkuu akamwuliza tena, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wake Mtukufu? 62 Yesu akasema, Mimi ndiye, nanyi mtamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kuume wa nguvu, akija na mawingu ya mbinguni. 63 Kuhani Mkuu akararua nguo zake, akisema, Tuna haja gani tena ya mashahidi? 64 Mmesikia kufuru yake; mwaonaje ninyi? Wote wakamhukumu kuwa imempasa kuuawa. 65 Wengine wakaanza kumtemea mate, wakamfunika uso, na kumpiga makonde, na kumwambia, tabiri. Hata watumishi nao wakampiga makofi. 66 Na Petro alikuwa chini behewani; akaja mmoja wa vijakazi wa Kuhani Mkuu, 67 akamwona Petro akikota moto; akamkazia macho, akasema, Wewe nawe ulikuwapo pamoja na yule Mnazareti, Yesu. 68 Akakana, akasema, Sijui wala sisikii unayoyasema wewe. Akatoka nje hata ukumbini; jogoo akawika. 69 Na yule kijakazi akamwona tena, akaanza tena kuwaambia waliosimama pale, Huyu ni mmoja wao. 70 Akakana tena. Kitambo kidogo tena wale waliosimama pale wakamwambia Petro, Hakika u mmoja wao, kwa sababu u Mgalilaya wewe. 71 Akaanza kulaani na kuapiza, Simjui mtu huyu mnayemnena. 72 Na mara jogoo akawika mara ya pili. Petro akalikumbuka lile neno aliloambiwa na Yesu, Kabla ya kuwika jogoo mara mbili, utanikana mara tatu. Na alipolifikiri, akalia.

Marko 15

1 Mara kulipokuwa asubuhi wakuu wa makuhani walifanya shauri pamoja na wazee na waandishi na baraza nzima, wakamfunga Yesu, wakamchukua, wakamleta mbele ya Pilato. 2 Pilato akamwuliza, Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi? Akajibu, akamwambia, Wewe wasema. 3 Nao wakuu wa makuhani walikuwa wakimshitaki mambo mengi. 4 Pilato akamwuliza tena akisema, Hujibu neno? Tazama ni mambo mangapi wanayokushitaki! 5 Wala Yesu hakujibu neno tena, hata Pilato akastaajabu. 6 Basi wakati wa sikukuu huwafungulia mfungwa mmoja, wamwombaye. 7 Palikuwa na mtu aitwaye Baraba, amefungwa pamoja na watu waliofanya fitina, na kufanya uuaji katika fitina ile. 8 Makutano wakaja, wakaanza kuomba awafanyie kama vile alivyozoea. 9 Pilato akawajibu, akisema, Je! Mnataka niwafungulie mfalme wa Wayahudi? 10 Kwa maana alitambua ya kuwa wakuu wa makuhani wamemtoa kwa husuda. 11 Lakini wakuu wa makuhani wakawataharakisha makutano, kwamba afadhali awafungulie Baraba. 12 Pilato akajibu tena akawaambia, Basi nimtendeje huyu mnayemnena kuwa ni mfalme wa Wayahudi? 13 Wakapiga kelele tena, Msulibishe. 14 Pilato akawaambia, Kwani, ni ubaya gani alioutenda? Wakazidi sana kupiga kelele, Msulibishe. 15 Pilato akipenda kuwaridhisha makutano, akawafungulia Baraba; akamtoa Yesu, baada ya kumpiga mijeledi, ili asulibiwe. 16 Nao askari wakamchukua ndani ya behewa, ndiyo Praitorio (yaani, nyumba ya uliwali), wakakusanya pamoja kikosi kizima. 17 Wakamvika vazi la rangi ya zambarau, wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani; 18 wakaanza kumsalimu, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! 19 Wakampiga mwanzi wa kichwa, wakamtemea mate, wakapiga magoti, wakamsujudia. 20 Hata wakiisha kumdhihaki, wakamvua lile vazi la rangi ya zambarau, wakamvika mavazi yake mwenyewe; wakamchukua nje ili wamsulibishe. 21 Wakamshurutisha mtu aliyekuwa akipita, akitoka mashamba, Simoni Mkirene, baba yao Iskanda na Rufo, ili auchukue msalaba wake. 22 Wakamleta mpaka mahali paitwapo Golgotha, yaani, Fuvu la kichwa. 23 Wakampa mvinyo iliyotiwa manemane, asiipokee. 24 Wakamsulibisha, wakagawa mavazi yake, wakayapigia kura kila mtu atwae nini. 25 Basi ilikuwa saa tatu, nao wakamsulibisha. 26 Palikuwa na anwani ya mashitaka yake iliyoandikwa juu, MFALME WA WAYAHUDI. 27 Na pamoja naye walisulibisha wanyang'anyi wawili, mmoja mkono wake wa kuume na mmoja mkono wake wa kushoto. 28 Basi andiko likatimizwa linenalo, Alihesabiwa pamoja na waasi. 29 Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa, wakisema, Ahaa! Wewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga katika siku tatu, 30 jiponye nafsi yako, ushuke msalabani. 31 Kadhalika na wakuu wa makuhani wakamdhihaki wao kwa wao, pamoja na waandishi, wakisema, Aliponya wengine; hawezi kujiponya mwenyewe. 32 Kristo, mfalme wa Israeli, na ashuke sasa msalabani tupate kuona na kuamini. Hata wale waliosulibiwa pamoja naye wakamfyolea. 33 Na ilipokuwa saa sita, palikuwa na giza juu ya nchi yote, hata saa tisa. 34 Na saa tisa Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Maana yake, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? 35 Na baadhi yao waliosimama pale, walisema, Tazama, anamwita Eliya. 36 Na mmoja akaenda mbio, akajaza sifongo siki, akaitia juu ya mwanzi, akamnywesha, akisema, Acheni, na tuone kwamba Eliya anakuja kumtelemsha. 37 Naye Yesu akatoa sauti kuu, akakata roho. 38 Pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini. 39 Basi yule akida, aliyesimama hapo akimwelekea, alipoona ya kuwa alikata roho jinsi hii, akasema, Hakika mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu. 40 Palikuwako na wanawake wakitazama kwa mbali; miongoni mwao alikuwamo Mariamu Magdalene, na Mariamu mama yao Yakobo mdogo na Yose, na Salome; 41 hao ndio waliofuatana naye huko Galilaya, na kumtumikia; na wengine wengi waliopanda pamoja naye mpaka Yerusalemu. 42 Hata ikiisha kuwa jioni, kwa sababu ni Maandalio, ndiyo siku iliyo kabla ya sabato, 43 akaenda Yusufu, mtu wa Arimathaya, mstahiki, mtu wa baraza ya mashauri, naye mwenyewe anautazamia ufalme wa Mungu; akafanya ujasiri, akaingia mbele ya Pilato akauomba mwili wake Yesu. 44 Lakini Pilato akastaajabu, kwamba amekwisha kufa. Akamwita yule akida, akamwuliza kwamba amekufa kitambo. 45 Hata alipokwisha kupata hakika kwa yule akida, alimpa Yusufu yule maiti. 46 Naye akanunua sanda ya kitani, akamtelemsha, akamfungia ile sanda, akamweka katika kaburi lililochongwa mwambani; akavingirisha jiwe mbele ya mlango wa kaburi. 47 Nao Mariamu Magdalene na Mariamu mamaye Yose wakapatazama mahali alipowekwa.

Marko 16

1 Hata sabato ilipokwisha kupita, Mariamu Magdalene na Mariamu mamaye Yakobo, na Salome walinunua manukato wapate kwenda kumpaka. 2 Hata alfajiri mapema, siku ya kwanza ya juma, wakaenda kaburini, jua lilipoanza kuchomoza; 3 wakasemezana wao kwa wao, Ni nani atakayetuvingirishia lile jiwe mlangoni pa kaburi? 4 Hata walipotazama, waliona ya kuwa lile jiwe limekwisha kuvingirishwa; nalo lilikuwa kubwa mno. 5 Wakaingia kaburini wakaona kijana ameketi upande wa kuume, amevaa vazi jeupe; wakastaajabu. 6 Naye akawaambia, Msistaajabu; mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyesulibiwa; amefufuka; hayupo hapa; patazameni mahali walipomweka. 7 Lakini enendeni zenu, mkawaambie wanafunzi wake, na Petro, ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya; huko mtamwona, kama alivyowaambia. 8 Wakatoka nje, wakakimbia kutoka kaburini; kwa maana wameingia tetemeko na ushangao; wala hawakumwambia mtu neno, maana waliogopa. 9 Naye alipofufuka alfajiri siku ya kwanza ya juma, alimtokea kwanza Mariamu Magdalene, ambaye kwamba alimtoa pepo saba. 10 Huyo akashika njia akawapasha habari wale waliokuwa pamoja naye, nao wakali wanaomboleza na kulia. 11 Walakini hao waliposikia kama yu hai, naye amemwona, hawakusadiki. 12 Baada ya hayo akawatokea watu wawili miongoni mwao, ana sura nyingine; nao walikuwa wakishika njia kwenda shamba. 13 Na hao wakaenda zao wakawapa habari wale wengine; wala hao hawakuwasadiki. 14 Baadaye akaonekana na wale kumi na mmoja walipokuwa wakila, akawakemea kwa kutokuamini kwao na ugumu wa mioyo yao, kwa kuwa hawakuwasadiki wale waliomwona alipofufuka katika wafu. 15 Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. 16 Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. 17 Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; 18 watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya. 19 Basi Bwana Yesu, baada ya kusema nao, akachukuliwa juu mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. 20 Nao wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.

Luka 1

1 Kwa kuwa watu wengi wametia mikono kutunga kwa taratibu habari za mambo yale yaliyotimizwa katikati yetu, 2 kama walivyotuhadithia wale waliokuwa mashahidi wenye kuyaona, na watumishi wa lile neno tokea mwanzo, 3 nimeona vema mimi nami, kwa kuwa nimejitafutia usahihi wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu, Theofilo mtukufu, 4 upate kujua hakika ya mambo yale uliyofundishwa. 5 Zamani za Herode, mfalme wa Uyahudi, palikuwa na kuhani mmoja, jina lake Zakaria, wa zamu ya Abiya, na mkewe alikuwa mmojawapo wa uzao wa Haruni, jina lake Elisabeti. 6 Na wote wawili walikuwa wenye haki mbele za Mungu, wakiendelea katika amri zote za Bwana na maagizo yake bila lawama. 7 Nao walikuwa hawana mtoto, maana Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili ni wazee sana. 8 Basi ikawa, alipokuwa akifanya kazi ya ukuhani katika taratibu ya zamu yake mbele za Mungu, 9 kama ilivyokuwa desturi ya ukuhani, kura ilimwangukia kuingia katika hekalu la Bwana ili kufukiza uvumba. 10 Na makutano yote ya watu walikuwa wakisali nje saa ya kufukiza uvumba. 11 Akatokewa na malaika wa Bwana, amesimama upande wa kuume wa madhabahu ya kufukizia. 12 Zakaria alipomwona alifadhaika, hofu ikamwingia. 13 Lakini yule malaika akamwambia, Usiogope, Zakaria, maana dua yako imesikiwa, na mkeo Elisabeti atakuzalia mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yohana. 14 Nawe utakuwa na furaha na shangwe, na watu wengi watakufurahia kuzaliwa kwake. 15 Kwa sababu atakuwa mkuu mbele za Bwana; hatakunywa divai wala kileo; naye atajazwa Roho Mtakatifu hata tangu tumboni mwa mamaye. 16 Na wengi katika Waisraeli atawarejeza kwa Bwana Mungu wao. 17 Naye atatangulia mbele zake katika roho ya Eliya, na nguvu zake, ili kuigeuza mioyo ya baba iwaelekee watoto, na kuwatilia waasi akili za wenye haki, na kumwekea Bwana tayari watu waliotengenezwa. 18 Zakaria akamwambia malaika, Nitajuaje neno hilo? Maana mimi ni mzee, na mke wangu ni mkongwe wa siku nyingi. 19 Malaika akamjibu akamwambia, Mimi ni Gabrieli, nisimamaye mbele za Mungu; nami nimetumwa niseme nawe, na kukupasha habari hizi njema. 20 Na tazama! Utakuwa bubu, usiweze kusema, mpaka siku ile yatakapotukia hayo, kwa sababu hukuyasadiki maneno yangu; nayo yatatimizwa kwa wakati wake. 21 Na wale watu walikuwa wakimngojea Zakaria, wakastaajabia kukawia kwake mle hekaluni. 22 Alipotoka hali hawezi kusema nao, walitambua ya kuwa ameona maono ndani ya hekalu, naye aliendelea kuwaashiria akakaa bubu. 23 Ikawa siku za huduma yake zilipokuwa zimetimia akaenda nyumbani kwake. 24 Hata baada ya siku zile mkewe Elisabeti alichukua mimba akatawa miezi mitano, akisema, 25 Hivi ndivyo alivyonitendea Bwana katika siku zile alizoniangalia ili kuniondolea aibu yangu mbele ya watu. 26 Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, 27 kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu. 28 Akaingia nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. 29 Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? 30 Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. 31 Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. 32 Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. 33 Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho. 34 Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? 35 Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. 36 Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; 37 kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu. 38 Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema. Kisha malaika akaondoka akaenda zake. 39 Basi, Mariamu akaondoka siku hizo, akaenda hata nchi ya milimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, 40 akaingia nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elisabeti. 41 Ikawa Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani ya tumbo lake; Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu; 42 akapaza sauti kwa nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako amebarikiwa. 43 Limenitokeaje neno hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi? 44 Maana sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu. 45 Naye heri aliyesadiki; kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana. 46 Mariamu akasema, Moyo wangu wamwadhimisha Bwana, 47 Na roho yangu imemfurahia Mungu, Mwokozi wangu; 48 Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa; 49 Kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea makuu, Na jina lake ni takatifu. 50 Na rehema zake hudumu vizazi hata vizazi Kwa hao wanaomcha. 51 Amefanya nguvu kwa mkono wake; Amewatawanya walio na kiburi katika mawazo ya mioyo yao; 52 Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza. 53 Wenye njaa amewashibisha mema, Na wenye mali amewaondoa mikono mitupu. 54 Amemsaidia Israeli, mtumishi wake; Ili kukumbuka rehema zake; 55 Kama alivyowaambia baba zetu, Ibrahimu na uzao wake hata milele. 56 Mariamu akakaa naye kadiri ya miezi mitatu, kisha akarudi kwenda nyumbani kwake. 57 Ikawa, siku za kuzaa kwake Elisabeti zilipotimia, alizaa mtoto mwanamume. 58 Wakasikia jirani zake na jamaa zake ya kwamba Bwana amemwongezea rehema zake, wakafurahi pamoja naye. 59 Ikawa siku ya nane wakaja kumtahiri mtoto; wakataka kumpa jina la babaye, Zakaria. 60 Mamaye akajibu akasema La, sivyo; bali, ataitwa Yohana. 61 Wakamwambia, Hapana mtu katika jamaa zako aitwaye jina hilo. 62 Wakamwashiria babaye wajue atakavyo kumwita. 63 Akataka kibao, akaandika ya kwamba, Jina lake ni Yohana. Wakastaajabu wote. 64 Papo hapo kinywa chake kikafunguliwa na ulimi wake pia, akaanza kunena akimsifu Mungu. 65 Wakaingiwa na hofu wote waliokuwa wakikaa karibu nao; na mambo hayo yote yakatangazwa katika nchi yote ya milima milima ya Uyahudi. 66 Na wote walioyasikia wakayaweka mioyoni mwao, wakisema, Mtoto huyu atakuwa wa namna gani? Kwa sababu mkono wa Bwana ulikuwa pamoja naye. 67 Na Zakaria, baba yake, akajazwa Roho Mtakatifu, akatabiri, akisema, 68 Atukuzwe Bwana, Mungu wa Israeli, Kwa kuwa amewajia watu wake, na kuwakomboa. 69 Ametusimamishia pembe ya wokovu Katika mlango wa Daudi, mtumishi wake. 70 Kama alivyosema tangu mwanzo Kwa kinywa cha manabii wake watakatifu; 71 Tuokolewe na adui zetu Na mikononi mwao wote wanaotuchukia; 72 Ili kuwatendea rehema baba zetu, Na kulikumbuka agano lake takatifu; 73 Uapo aliomwapia Ibrahimu, baba yetu, 74 Ya kwamba atatujalia sisi, Tuokoke mikononi mwa adui zetu, Na kumwabudu pasipo hofu, 75 Kwa utakatifu na kwa haki Mbele zake siku zetu zote. 76 Nawe, mtoto, utaitwa nabii wake Aliye juu, Kwa maana utatangulia mbele za uso wa Bwana umtengenezee njia zake; 77 Uwajulishe watu wake wokovu, Katika kusamehewa dhambi zao. 78 Kwa njia ya rehema za Mungu wetu, Ambazo kwa hizo mwangaza utokao juu umetufikia, 79 Kuwaangaza wakaao katika giza na uvuli wa mauti, Na kuiongoza miguu yetu kwenye njia ya amani. 80 Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu rohoni, akakaa majangwani hata siku ya kutokea kwake kwa Israeli.

Luka 2

1 Siku zile amri ilitoka kwa Kaisari Augusto ya kwamba iandikwe orodha ya majina ya watu wote wa ulimwengu. 2 Orodha hii ndiyo ya kwanza iliyoandikwa hapo Kirenio alipokuwa liwali wa Shamu. 3 Watu wote wakaenda kuandikwa, kila mtu mjini kwao. 4 Yusufu naye aliondoka Galilaya, toka mji wa Nazareti, akapanda kwenda Uyahudi mpaka mji wa Daudi, uitwao Bethlehemu, kwa kuwa yeye ni wa mbari na jamaa ya Daudi; 5 ili aandikwe pamoja na Mariamu mkewe, ambaye amemposa, naye ana mimba. 6 Ikawa, katika kukaa huko, siku zake za kuzaa zikatimia, 7 akamzaa mwanawe, kifungua mimba, akamvika nguo za kitoto, akamlaza katika hori ya kulia ng'ombe, kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba ya wageni. 8 Na katika nchi ile ile walikuwako wachungaji wakikaa makondeni na kulinda kundi lao kwa zamu usiku. 9 Malaika wa Bwana akawatokea ghafula, utukufu wa Bwana ukawang'aria pande zote, wakaingiwa na hofu kuu. 10 Malaika akawaambia, Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote; 11 maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana. 12 Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hori ya kulia ng'ombe. 13 Mara walikuwapo pamoja na huyo malaika, wingi wa jeshi la mbinguni, wakimsifu Mungu, na kusema, 14 Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia. 15 Ikawa, malaika hao walipoondoka kwenda zao mbinguni, wale wachungaji waliambiana, Haya, na twendeni mpaka Bethlehemu, tukalione hilo lililofanyika, alilotujulisha Bwana. 16 Wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini. 17 Walipomwona wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto. 18 Wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji. 19 Lakini Mariamu akayaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake. 20 Wale wachungaji wakarudi, huku wanamtukuza Mungu na kumsifu kwa mambo yote waliyosikia na kuyaona, kama walivyoambiwa. 21 Hata zilipotumia siku nane za kumtahiri, aliitwa jina lake Yesu; kama alivyoitwa na malaika kabla hajachukuliwa mimba. 22 Kisha, zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa walikwenda naye hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana, 23 (kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana), 24 wakatoe na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana, Hua wawili au makinda ya njiwa wawili. 25 Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. 26 Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. 27 Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, 28 yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, 29 Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; 30 Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, 31 Uliouweka tayari machoni pa watu wote; 32 Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli. 33 Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. 34 Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. 35 Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi. 36 Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume miaka saba baada ya uanawali wake. 37 Naye ni mjane wa miaka themanini na minne; haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba. 38 Huyu alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi katika Yerusalemu akawatolea habari zake. 39 Basi, walipokwisha kuyatimiza yote kama yalivyoagizwa katika sheria ya Bwana, walirejea Galilaya mpaka mjini kwao, Nazareti. 40 Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake. 41 Basi, wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka. 42 Na alipopata umri wake miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; 43 na walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. 44 Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao; 45 na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. 46 Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47 Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake. 48 Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni. 49 Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu? 50 Nao hawakuelewa na neno hilo alilowaambia. 51 Akashuka pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; na mamaye aliyaweka hayo yote moyoni mwake. 52 Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.

Luka 3

1 Mwaka wa kumi na tano wa kutawala kwake Kaisari Tiberio, Pontio Pilato alipokuwa liwali wa Uyahudi, na Herode mfalme wa Galilaya, na Filipo, ndugu yake, mfalme wa Iturea na nchi ya Trakoniti, na Lisania mfalme wa Abilene, 2 wakati wa ukuhani mkuu wa Anasi na Kayafa, neno la Mungu lilimfikia Yohana, mwana wa Zakaria, jangwani. 3 Akafika nchi yote iliyo karibu na Yordani, akihubiri ubatizo wa toba liletalo ondoleo la dhambi, 4 kama ilivyoandikwa katika chuo cha maneno ya nabii Isaya; Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake. 5 Kila bonde litajazwa, Na kila mlima na kilima kitashushwa; Palipopotoka patakuwa pamenyoka, Na palipoparuza patalainishwa; 6 Na wote wenye mwili watauona wokovu wa Mungu. 7 Basi, aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? 8 Basi, toeni matunda yapatanayo na toba; wala msianze kusema mioyoni mwenu, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumwinulia Ibrahimu watoto. 9 Na sasa hivi shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni. 10 Makutano wakamwuliza, Tufanye nini basi? 11 Akawajibu akiwaambia, Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu; na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo. 12 Watoza ushuru nao wakaja kubatizwa, wakamwuliza, Mwalimu, tufanye nini sisi? 13 Akawaambia, Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa. 14 Askari nao wakamwuliza, wakisema, Sisi nasi tufanye nini? Akawaambia, Msidhulumu mtu, wala msishitaki kwa uongo; tena mtoshewe na mshahara wenu. 15 Basi, watu walipokuwa wakingoja yatakayotokea, wote wakiwaza-waza mioyoni mwao habari za Yohana, kama labda yeye ndiye Kristo, 16 Yohana alijibu akawaambia wote, Kweli mimi nawabatiza kwa maji; lakini yuaja mtu mwenye nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto; 17 ambaye pepeo lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake, na kuikusanya ngano ghalani mwake, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika. 18 Basi, kwa maonyo mengine mengi aliwahubiri watu. 19 Lakini mfalme Herode alipokaripiwa na yeye kwa ajili ya Herodia, mke wa nduguye, na maovu yote aliyoyafanya Herode, 20 aliongeza na hili juu ya yote, alimfunga Yohana gerezani. 21 Ikawa, watu wote walipokwisha kubatizwa, na Yesu naye amebatizwa, naye anaomba, mbingu zilifunuka; 22 Roho Mtakatifu akashuka juu yake kwa mfano wa kiwiliwili, kama hua; sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe. 23 Na Yesu mwenyewe, alipoanza kufundisha, alikuwa amepata umri wake kama miaka thelathini, akidhaniwa kuwa ni mwana wa Yusufu, wa Eli, 24 wa Mathati, wa Lawi, wa Melki, wa Yana, wa Yusufu, 25 wa Matathia, wa Amosi, wa Nahumu, wa Esli, wa Nagai, 26 wa Maathi, wa Matathia, wa Semei, wa Yusufu, wa Yuda, 27 wa Yoana, wa Resa, wa Zerubabeli, wa Shealtieli, wa Neri, 28 wa Melki, wa Adi, wa Kosamu, wa Elmadamu, wa Eri, 29 wa Yoshua, wa Eliezeri, wa Yorimu, wa Mathati, wa Lawi, 30 wa Simeoni, wa Yuda, wa Yusufu, wa Yonamu, wa Eliakimu, 31 wa Melea, wa Mena, wa Matatha, wa Nathani, wa Daudi, 32 wa Yese, wa Obedi, wa Boazi, wa Salmoni, wa Nashoni, 33 wa Aminadabu, wa Aramu, wa Hesroni, wa Peresi, wa Yuda, 34 wa Yakobo, wa Isaka, wa Ibrahimu, wa Tera, wa Nahori, 35 wa Serugi, wa Ragau, wa Pelegi, wa Eberi, wa Sala, 36 wa Kenani, wa Arfaksadi, wa Shemu, wa Nuhu, wa Lameki, 37 wa Methusela, wa Henoko, wa Yaredi, wa Mahalaleli, wa Kenani, 38 wa Enoshi, wa Sethi, wa Adamu, wa Mungu.

Luka 4

1 Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani, 2 akijaribiwa na Ibilisi. Na siku hizo alikuwa hali kitu; hata zilipotimia, aliona njaa. 3 Ibilisi akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate. 4 Yesu akamjibu, Imeandikwa ya kwamba mtu hataishi kwa mkate tu. 5 Akampandisha juu, akamwonyesha milki zote za ulimwengu kwa dakika moja. 6 Ibilisi akamwambia, Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa ye yote kama nipendavyo. 7 Basi, wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako. 8 Yesu akajibu akamwambia, Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. 9 Akamwongoza mpaka Yerusalemu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, jitupe chini; 10 kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake wakulinde; 11 na ya kwamba,mikononi mwao watakuchukua, Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe. 12 Yesu akajibu akamwambia, Imenenwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako. 13 Basi alipomaliza kila jaribu, Ibilisi akamwacha akaenda zake kwa muda. 14 Yesu akarudi kwa nguvu za Roho, akenda Galilaya; habari zake zikaenea katika nchi zote za kandokando. 15 Naye alikuwa akifundisha katika masinagogi yao, akitukuzwa na watu wote. 16 Akaenda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ili asome. 17 Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, 18 Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, 19 Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa. 20 Akakifunga chuo, akamrudishia mtumishi, akaketi; na watu wote waliokuwamo katika sinagogi wakamkazia macho. 21 Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu. 22 Wakamshuhudia wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu? 23 Akawaambia, Hapana shaka mtaniambia mithali hii, Tabibu, jiponye nafsi yako; mambo yote tuliyosikia kwamba yametendeka Kapernaumu, yatende na hapa pia katika nchi yako mwenyewe. 24 Akasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe. 25 Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; 26 wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni. 27 Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu. 28 Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo. 29 Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; 30 lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake. 31 Akashuka mpaka Kapernaumu, mji wa Galilaya, akawa akiwafundisha siku ya sabato; 32 wakashangaa mno kwa mafundisho yake, kwa kuwa neno lake lilikuwa na uwezo. 33 Na ndani ya sinagogi mlikuwa na mtu mwenye roho ya pepo mchafu, akalia kwa sauti kuu, 34 akisema, Acha! Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu. 35 Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha katikati, akamtoka asimdhuru neno. 36 Mshangao ukawashika wote, wakasemezana wakisema, Ni neno gani hili, maana awaamuru pepo wachafu kwa uwezo na nguvu, nao hutoka. 37 Habari zake zikaenea kila mahali katika nchi ile. 38 Akatoka katika sinagogi, akaingia katika nyumba ya Simoni. Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa ameshikwa na homa kali, wakamwomba kwa ajili yake. 39 Akasimama karibu naye, akaikemea ile homa, ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia. 40 Na jua lilipokuwa likichwa, wote waliokuwa na wagonjwa wenye maradhi mbali mbali waliwaleta kwake, akaweka mikono yake juu ya kila mmoja akawaponya. 41 Pepo nao waliwatoka watu wengi, wakipiga kelele na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu. Akawakemea, asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo. 42 Hata kulipokucha alitoka akaenda mahali pasipokuwa na watu; makutano wakawa wakimtafuta-tafuta, wakafika kwake, wakataka kumzuia asiondoke kwao. 43 Akawaambia, Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa. 44 Basi, alikuwa akihubiri katika masinagogi ya Galilaya.

Luka 5

1 Ikawa makutano walipomsonga wakilisikiliza neno la Mungu, yeye alikuwa amesimama kando ya ziwa la Genesareti, 2 akaona vyombo viwili vimekaa kando ya ziwa, lakini wavuvi wametoka, wanaosha nyavu zao. 3 Akaingia katika chombo kimoja, ndicho chake Simoni, akamtaka akipeleke mbali kidogo na pwani. Akaketi, akawafundisha makutano ali chomboni. 4 Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki. 5 Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu. 6 Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika; 7 wakawapungia mikono washirika wao waliokuwa katika chombo cha pili, waje kuwasaidia; wakaja, wakavijaza vyombo vyote viwili, hata vikataka kuzama. 8 Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana. 9 Maana alishikwa na ushangao, yeye na wote waliokuwa pamoja naye, kwa sababu ya wingi wa samaki walioupata; 10 na kadhalika Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, waliokuwa washirika wa Simoni. Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu. 11 Hata walipokwisha kuviegesha pwani vyombo vyao, wakaacha vyote wakamfuata. 12 Ikawa, alipokuwa katika mmojawapo wa miji ile, tazama, palikuwa na mtu amejaa ukoma; naye alipomwona Yesu alianguka kifudifudi, akamwomba akisema, Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa. 13 Naye akaunyosha mkono wake, akamgusa akisema, Nataka; takasika. Na mara ukoma wake ukamwondoka. 14 Akamkataza asimwambie mtu, ila, Nenda ukajionyeshe kwa kuhani; ukatoe kwa ajili ya kutakasika kwako kama Musa alivyoamuru, iwe ushuhuda kwao. 15 Lakini habari zake zikazidi kuenea, wakakutanika makutano mengi wamsikilize na kuponywa magonjwa yao. 16 Lakini yeye alikuwa akijiepua, akaenda mahali pasipokuwa na watu, akaomba. 17 Ikawa siku zile mojawapo alikuwa akifundisha, na Mafarisayo na waalimu wa torati walikuwa wameketi hapo, waliotoka katika kila kijiji cha Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu; na uweza wa Bwana ulikuwapo apate kuponya. 18 Na tazama, wakaja watu wanamchukua kitandani mtu mwenye kupooza; wakataka kumpeleka ndani na kumweka mbele yake. 19 Hata walipokosa nafasi ya kumpeleka ndani kwa ajili ya lile kundi la watu, walipanda juu ya dari wakampisha katika matofali ya juu, wakamshusha yeye na kitanda chake katikati mbele ya Yesu. 20 Naye alipoiona imani yao, alimwambia, Ee rafiki, umesamehewa dhambi zako. 21 Basi, wale waandishi na Mafarisayo wakaanza kuhojiana wakisema, Ni nani huyu asemaye maneno ya kukufuru? N'nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake? 22 Na Yesu alijua hoja zao, akajibu akawaambia, Mnahojiana nini mioyoni mwenu? 23 Lililo jepesi ni lipi? Kusema, Umesamehewa dhambi zako, au kusema, Ondoka, uende? 24 Lakini, mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (alimwambia yule mwenye kupooza). Nakuambia, Ondoka, ujitwike kitanda chako, ukaende zako nyumbani kwako. 25 Mara hiyo akasimama mbele yao, akajitwika kile alichokilalia, akaenda zake nyumbani kwake, huku akimtukuza Mungu. 26 Ushangao ukawashika wote, wakamtukuza Mungu; wakajaa hofu, wakisema, Leo tumeona mambo ya ajabu. 27 Baada ya hayo akatoka, akaona mtoza ushuru, jina lake Lawi, ameketi forodhani, akamwambia, Nifuate. 28 Akaacha vyote, akaondoka, akamfuata. 29 Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao. 30 Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? 31 Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. 32 Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu. 33 Nao wakamwambia, Wanafunzi wa Yohana hufunga mara nyingi, na kuomba dua; na kadhalika wanafunzi wa Mafarisayo; lakini wanafunzi wako hula na kunywa! 34 Lakini Yesu akawaambia, Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini, akiwapo bwana arusi pamoja nao? 35 Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi, ndipo watakapofunga siku zile. 36 Akawaambia na mithali, Hakuna akataye kiraka cha vazi jipya na kukitia katika vazi kuukuu; na kama akitia, amelikata lile jipya, na kile kiraka cha vazi jipya hakilingani na lile vazi kuukuu. 37 Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama akitia, ile divai mpya itavipasua vile viriba, divai yenyewe itamwagika, na viriba vitaharibika. 38 Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya. 39 Wala hakuna anywaye divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale ndiyo iliyo njema.

Luka 6

1 Ikawa siku ya sabato moja alikuwa akipita katika mashamba, wanafunzi wake wakawa wakivunja masuke na kuyala, wakiyapukusa-pukusa mikononi mwao. 2 Basi baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, Mbona mnafanya lisilo halali siku ya sabato? 3 Yesu akawajibu akawaambia, Hamkulisoma hata hilo alilolifanya Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wale aliokuwa nao? 4 Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaitwaa mikate ile ya Wonyesho, akaila akawapa na hao wenziwe, ambayo si halali kuila ila kwa makuhani peke yao. 5 Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato. 6 Ikawa siku ya sabato nyingine aliingia katika sinagogi akafundisha; na mlikuwamo mtu ambaye mkono wake wa kuume umepooza. 7 Na waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimvizia, ili waone kwamba ataponya siku ya sabato; kusudi wapate neno la kumshitakia. 8 Lakini yeye akayatambua mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati; akaondoka akasimama. 9 Ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza? 10 Akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena. 11 Wakajawa na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu. 12 Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. 13 Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume; 14 Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, 15 na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, 16 na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti. 17 Akashuka pamoja nao, akasimama mahali tambarare, pamoja na wanafunzi wake wengi, na makutano makubwa ya watu waliotoka Uyahudi wote na Yerusalemu, na pwani ya Tiro na Sidoni; waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao; 18 na wale waliosumbuliwa na pepo wachafu; waliponywa. 19 Na makutano yote walikuwa wakitaka kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa ukimtoka ukiwaponya wote. 20 Akainua macho yake akawatazama wanafunzi wake, akasema, Heri ninyi mlio maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu. 21 Heri ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba. Heri ninyi mliao sasa, kwa sababu mtacheka. 22 Heri ninyi watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu. 23 Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni, maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo. 24 Lakini, ole wenu ninyi mlio na mali, kwa kuwa faraja yenu mmekwisha kuipata. 25 Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa. Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa mtaomboleza na kulia. 26 Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo. 27 Lakini nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi, 28 wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi. 29 Akupigaye shavu moja, mgeuzie la pili, naye akunyang'anyaye joho yako, usimzuilie na kanzu. 30 Mpe kila akuombaye, na akunyang'anyaye vitu vyako, usitake akurudishie. 31 Na kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo. 32 Maana mkiwapenda wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi huwapenda wale wawapendao. 33 Nanyi mkiwatendea mema wale wawatendeao mema, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo. 34 Na mkiwakopesha watu huku mkitumaini kupata kitu kwao, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi, ili warudishiwe vile vile. 35 Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu. 36 Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. 37 Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa; msilaumu, nanyi hamtalaumiwa; achilieni, nanyi mtaachiliwa. 38 Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa. 39 Akawaambia mithali, Je! Aliye kipofu aweza kuongoza kipofu? Hawatatumbukia shimoni wote wawili? 40 Mwanafunzi hawi mkuu kuliko mwalimu wake, lakini kila mtu ambaye amehitimu hulingana na mwalimu wake. 41 Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? 42 Au, utawezaje kumwambia ndugu yako, Ndugu yangu, niache nikitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho lako, nawe huiangalii boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi kilichomo katika jicho la ndugu yako. 43 Kwa maana hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; 44 kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu. 45 Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake. 46 Na kwa nini mnaniita, Bwana, Bwana, walakini hamyatendi nisemayo? 47 Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. 48 Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri. 49 Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa.

Luka 7

1 Alipokwisha kuyamaliza maneno yake yote masikioni mwa watu, aliingia Kapernaumu. 2 Na mtumwa wake akida mmoja alikuwa hawezi, karibu na kufa; naye ni mtu aliyempenda sana. 3 Aliposikia habari za Yesu, alituma wazee wa Wayahudi kwake kumwomba aje amponye mtumwa wake. 4 Nao walipofika kwa Yesu, walimsihi sana wakisema, Amestahili huyu umtendee neno hili; 5 maana, analipenda taifa letu, naye alitujengea sinagogi. 6 Basi Yesu akaenda pamoja nao. Hata alipokuwa si mbali na nyumba yake, yule akida alituma rafiki kwake, akamwambia, Bwana, usijisumbue, maana mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu; 7 kwa hiyo nilijiona sistahili mwenyewe kuja kwako; lakini, sema neno tu, na mtumwa wangu atapona. 8 Kwa maana mimi nami ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, mwenye askari chini yangu; nikimwambia huyu, Nenda, huenda; na huyu, Njoo, huja; na mtumwa wangu, Fanya hivi, hufanya. 9 Yesu aliposikia hayo alimstaajabia, akaugeukia mkutano uliokuwa ukimfuata, akasema, Nawaambia, hata katika Israeli sijaona imani kubwa namna hii. 10 Na wale waliotumwa waliporudi nyumbani, wakamkuta yule mtumwa ni mzima. 11 Baadaye kidogo alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa. 12 Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye. 13 Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie. 14 Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. 15 Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake. 16 Hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Nabii mkuu ametokea kwetu; na, Mungu amewaangalia watu wake. 17 Habari hii yake ikaenea katika Uyahudi wote, na katika nchi zote za kando kando. 18 Wanafunzi wa Yohana wakamletea habari za hayo yote. 19 Ndipo Yohana alipowaita wawili katika wanafunzi wake, akawatuma kwa Yesu akiuliza, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? 20 Nao walipofika kwake, walisema, Yohana Mbatizaji ametutuma kwako, akisema, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? 21 Na saa ile ile aliwaponya wengi magonjwa yao, na misiba, na pepo wabaya; na vipofu wengi aliwakirimia kuona. 22 Ndipo alipojibu, akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia; vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini wanahubiriwa habari njema. 23 Naye heri mtu ye yote asiyechukizwa nami. 24 Basi, wajumbe wa Yohana walipokwisha ondoka, alianza kuwaambia makutano habari za Yohana, Mlitoka kwenda nyikani kutazama nini? Unyasi ukitikiswa na upepo? 25 Lakini mlitoka kwenda kuona nini? Mtu aliyevikwa mavazi mororo? Jueni, watu wenye mavazi ya utukufu, wanaokula raha, wamo katika majumba ya kifalme. 26 Lakini, mlitoka kwenda kuona nini? Nabii? Naam, nawaambia, na aliye zaidi ya nabii. 27 Huyo ndiye aliyeandikiwa haya, Tazama, namtuma mjumbe wangu Mbele ya uso wako, Atakayeitengeneza njia yako mbele yako. 28 Nami nawaambia, Katika wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana; lakini aliye mdogo katika ufalme wa Mungu ni mkuu kuliko yeye. 29 Na watu wote na watoza ushuru waliposikia hayo, waliikiri haki ya Mungu, kwa kuwa wamebatizwa kwa ubatizo wa Yohana. 30 Lakini, Mafarisayo na wana-sheria walilipinga shauri la Mungu juu yao, kwa kuwa hawakubatizwa naye. 31 Bwana akasema, Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki? Nao wamefanana na nini? 32 Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia. 33 Kwa kuwa Yohana Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, Ana pepo. 34 Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa; nanyi mwasema, Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi. 35 Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa watoto wake wote. 36 Mtu mmoja katika Mafarisayo alimwalika ale chakula kwake; akaingia katika nyumba yake yule Farisayo, akaketi chakulani. 37 Na tazama, mwanamke mmoja wa mji ule, aliyekuwa mwenye dhambi, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu. 38 Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea miguu machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu. 39 Basi, yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani, ya kwamba ni mwenye dhambi. 40 Yesu akajibu akamwambia, Simoni, nina neno nitakalo kukuambia. Akasema, Mwalimu, nena. 41 Akasema, Mtu mmoja mkopeshaji alikuwa na wadeni wawili; mmoja amwia dinari mia tano, na wa pili hamsini. 42 Nao walipokuwa hawana cha kumlipa, aliwasamehe wote wawili. Katika hao wawili ni yupi atakayempenda zaidi? 43 Simoni akajibu akasema, Nadhani ni yule ambaye alimsamehe nyingi. Akamwambia, Umeamua haki. 44 Akamgeukia yule mwanamke, akamwambia Simoni, Wamwona mwanamke huyu? Niliingia nyumbani kwako, hukunipa maji kwa miguu yangu; bali huyu amenidondoshea machozi miguu yangu, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake. 45 Wewe hukunibusu; lakini huyu tangu nilipoingia hakuacha kunibusu sana miguu yangu. 46 Hukunipaka kichwa changu mafuta; bali huyu amenipaka miguu yangu marhamu. 47 Kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo hupenda kidogo. 48 Kisha alimwambia mwanamke, Umesamehewa dhambi zako. 49 Ndipo wale walioketi chakulani pamoja naye walianza kusema mioyoni mwao, Ni nani huyu hata asamehe dhambi? 50 Akamwambia yule mwanamke, Imani yako imekuokoa, enenda zako kwa amani.

Luka 8

1 Ikawa baada ya hayo alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, 2 na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, 3 na Yoana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao. 4 Mkutano mkuu ulipokutanika, na wale waliotoka kila mji wakimjia, alisema kwa mfano; 5 Mpanzi alitoka kwenda kupanda mbegu zake; naye alipokuwa akizipanda, nyingine zilianguka karibu na njia, zikakanyagwa, ndege wa angani wakazila. 6 Nyingine zikaanguka penye mwamba; zilipoanza kumea zikakauka kwa kukosa rutuba. 7 Nyingine zikaanguka kati ya miiba, na miiba ikamea pamoja nazo ikazisonga. 8 Nyingine zikaanguka penye udongo mzuri; zikamea, zikazaa moja kwa mia. Alipokuwa akinena hayo alipaza sauti akisema, Mwenye masikio ya kusikilia, na asikie. 9 Wanafunzi wake wakamwuliza, Maana yake nini mfano huo? 10 Akasema, Ninyi mmepewa kuzijua siri za ufalme wa Mungu; bali wengine kwa mifano, ili wakiona wasione, na wakisikia wasielewe. 11 Na huo mfano, maana yake ni hii; Mbegu ni neno la Mungu. 12 Wale wa karibu na njia ndio wasikiao, kisha huja Ibilisi akaliondoa hilo neno mioyoni mwao, wasije wakaamini na kuokoka. 13 Na wale penye mwamba ndio wale ambao wasikiapo hulipokea lile neno kwa furaha; nao hawana mizizi, huamini kitambo kidogo, na wakati wa kujaribiwa hujitenga. 14 Na zilizoanguka penye miiba ni wale waliosikia, na katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lo lote. 15 Na zile penye udongo mzuri, ndio wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno, na kulishika; kisha huzaa matunda kwa kuvumilia. 16 Hakuna mtu ambaye akiisha washa taa huifunika kwa chombo, au kuiweka mvunguni, bali huiweka juu ya kiango, ili waingiao wapate kuona nuru yake. 17 Kwa maana hakuna neno lililositirika ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa ambalo halitajulikana na kutokea wazi. 18 Jiangalieni basi jinsi msikiavyo; kwa kuwa mwenye kitu atapewa, na yule asiye na kitu atanyang'anywa hata kile ambacho anadhaniwa kuwa nacho. 19 Wakamwendea mama yake na ndugu zake, wasiweze kumkaribia kwa sababu ya mkutano. 20 Akaletewa habari akiambiwa, Mama yako na ndugu zako wamesimama nje wakitaka kuonana nawe. 21 Akawajibu akasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hao walisikiao neno la Mungu na kulifanya. 22 Ikawa siku zile mojawapo alipanda chomboni yeye na wanafunzi wake, akawaambia, Na tuvuke mpaka ng'ambo ya ziwa. Wakatweka matanga. 23 Nao walipokuwa wakienda, alilala usingizi. Ikashuka tufani juu ya ziwa, chombo kikaanza kujaa maji, wakawa katika hatari. 24 Wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana mkubwa, Bwana mkubwa, tunaangamia. Akaamka, akaukemea upepo na msukosuko wa maji, vikakoma; kukawa shwari. 25 Akawaambia, Imani yenu iko wapi? Wakaogopa, wakamaka, wakisema wao kwa wao, Ni nani huyu basi hata anaamuru upepo na maji, navyo vyamtii? 26 Wakafika pwani ya nchi ya Wagerasi, inayoelekea Galilaya. 27 Naye aliposhuka pwani, alikutana na mtu mmoja wa mji ule, mwenye pepo, hakuvaa nguo siku nyingi, wala hakukaa nyumbani, ila makaburini. 28 Alipomwona Yesu alipiga kelele, akaanguka mbele yake, akasema kwa sauti kuu, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakusihi usinitese. 29 Kwa kuwa amemwamuru yule pepo mchafu amtoke mtu yule. Maana amepagawa naye mara nyingi, hata alilindwa kifungoni na kufungwa minyororo na pingu; akavikata vile vifungo, akakimbizwa jangwani kwa nguvu za yule pepo. 30 Yesu akamwuliza, Jina lako nani? Akasema, Jina langu ni Jeshi; kwa sababu pepo wengi wamemwingia. 31 Wakamsihi asiwaamuru watoke kwenda shimoni. 32 Basi, hapo palikuwa na kundi la nguruwe wengi wakilisha mlimani; wakamsihi awape ruhusa kuwaingia wale. Akawapa ruhusa. 33 Pepo wakamtoka mtu yule wakawaingia nguruwe, nalo kundi lilitelemka gengeni kwa kasi, wakaingia ziwani, wakafa maji. 34 Wachungaji walipoona lililotokea walikimbia, wakaieneza habari mjini na mashambani. 35 Watu wakatoka kwenda kuliona lililotokea, wakamwendea Yesu, wakamwona mtu yule aliyetokwa na pepo ameketi miguuni pa Yesu, amevaa nguo, ana akili zake; wakaogopa. 36 Na wale waliokuwa wameona waliwaeleza jinsi alivyoponywa yule aliyepagawa na pepo. 37 Na jamii ya watu wa nchi ya Wagerasi iliyo kando kando walimwomba aondoke kwao, kwa kuwa walishikwa na hofu nyingi; basi akapanda chomboni, akarudi. 38 Na mtu yule aliyetokwa na pepo alimwomba ruhusa afuatane naye; lakini yeye alimwaga akisema, 39 Rudi nyumbani kwako, ukahubiri yalivyo makuu Mungu aliyokutendea. Akaenda zake, akihubiri katika mji wote, yalivyo makuu mambo aliyotendewa na Yesu. 40 Basi Yesu aliporudi mkutano ulimkaribisha kwa furaha, maana walikuwa wakimngojea wote. 41 Na tazama, mtu mmoja akaja, jina lake Yairo, naye ni mtu mkuu wa sinagogi, akaanguka miguuni pa Yesu, akamsihi aingie nyumbani kwake; 42 kwa kuwa binti yake yu katika kufa, ambaye ni mwana pekee, umri wake amepata miaka kumi na miwili. Na alipokuwa akienda makutano walimsonga. 43 Na mwanamke mmoja, ambaye ametokwa na damu muda wa miaka kumi na miwili, aliyekuwa amegharimiwa mali zake zote kwa kuwapa waganga asipate kuponywa na mtu ye yote, 44 alikwenda nyuma yake, akaugusa upindo wa vazi lake; na mara hiyo kutoka damu kwake kulikoma. 45 Yesu akasema, Ni nani aliyenigusa? Basi, watu wote walipokana, Petro alimwambia, Bwana mkubwa, makutano haya wanakuzunguka na kukusonga. 46 Yesu akasema, Mtu alinigusa, maana naona ya kuwa nguvu zimenitoka. 47 Yule mwanamke, alipoona ya kwamba hawezi kusitirika akaja akitetemeka, akaanguka mbele yake, akamweleza mbele ya watu wote sababu yake ya kumgusa, na jinsi alivyoponywa mara. 48 Akamwambia Binti, imani yako imekuponya; enenda zako na amani. 49 Alipokuwa akinena hayo, alikuja mtu kutoka nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akamwambia, Binti yako amekwisha kufa; usimsumbue mwalimu. 50 Lakini Yesu aliposikia hayo, alimjibu, Usiwe na hofu, amini tu, naye ataponywa. 51 Alipofika nyumbani hakuacha mtu kuingia pamoja naye ila Petro, na Yohana, na Yakobo, na babaye yule mtoto na mamaye. 52 Na watu wote walikuwa wakilia na kumwombolezea; akasema, Msilie, hakufa huyu, bali amelala usingizi tu. 53 Wakamcheka sana, maana walijua ya kuwa amekwisha kufa. 54 Akamshika mkono, akapaza sauti, akisema Kijana, inuka. 55 Roho yake ikamrejea, naye mara hiyo akasimama. Akaamuru apewe chakula. 56 Wazazi wake wakastaajabu sana, lakini akawakataza wasimwambie mtu lililotukia.

Luka 9

1 Akawaita wale Thenashara, akawapa uwezo na mamlaka juu ya pepo wote na kuponya maradhi. 2 Akawatuma wautangaze ufalme wa Mungu, na kupoza wagonjwa. 3 Akawaambia, Msichukue kitu kwa safari yenu, fimbo, wala mkoba, wala mkate, wala fedha, wala mmoja wenu asiwe na kanzu mbili. 4 Na nyumba yo yote mtakayoingia kaeni humo, mpaka mtoke mjini. 5 Na wale wasiowakaribisha, mtokapo katika mji huo, yakung'uteni hata mavumbi ya miguuni mwenu, kuwa ushuhuda juu yao. 6 Wakaenda, wakazunguka katika vijiji, wakihubiri injili, na kupoza watu kila mahali. 7 Na Herode mfalme akasikia habari za yote yaliyotendeka, akafadhaika kwa sababu watu wengine walisema ya kwamba Yohana amefufuka katika wafu, 8 na wengine ya kwamba Eliya ametokea, na wengine ya kwamba mmojawapo wa manabii wa kale amefufuka. 9 Lakini Herode akasema, Yohana nilimkata kichwa; basi ni nani huyu ambaye ninasikia mambo haya juu yake? Akataka kumwona. 10 Basi wale mitume waliporudi walimweleza mambo yote waliyoyatenda; akawachukua, akaenda nao faraghani mpaka mji mmoja uitwao Bethsaida. 11 Na makutano walipojua walimfuata; akawakaribisha, akawa akisema nao habari za ufalme wa Mungu, akawaponya wale wenye haja ya kuponywa. 12 Na jua likaanza kushuka; wakamwendea wale Thenashara, wakamwambia, Uage mkutano, ili waende katika vijiji na mashamba ya kandokando wapate mahali pa kulala na vyakula, maana hapa tulipo ni nyika tupu. 13 Akawaambia, Wapeni ninyi chakula. Wakasema, Hatuna kitu zaidi ya mikate mitano na samaki wawili, tusipokwenda tukawanunulie watu hawa wote vyakula. 14 Kwa kuwa wanaume waliokuwako walipata kama elfu tano. Akawaambia wanafunzi wake, Waketisheni watu kwa safu, kila safu watu hamsini. 15 Wakafanya hivyo, wakawaketisha wote. 16 Akaitwaa ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama juu mbinguni akavibariki, akavimega, akawapa wanafunzi wake ili wawaandikie mkutano. 17 Wakala, wakashiba wote; na katika vile vipande vilivyowabakia walikusanya vikapu kumi na viwili. 18 Ikawa alipokuwa akisali kwa faragha, wanafunzi wake walikuwapo pamoja naye, akawauliza, Je! Makutano hao wanasema ya kuwa mimi ni nani? 19 Wakamjibu wakisema, Yohana Mbatizaji; lakini wengine, Eliya; na wengine kwamba mmojawapo wa manabii wa kale amefufuka. 20 Akawaambia, Nanyi mwasema ya kwamba mimi ni nani? Petro akamjibu akasema, Ndiwe Kristo wa Mungu. 21 Akawaonya, akawakataza wasimwambie mtu neno hilo; 22 akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka. 23 Akawaambia wote, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. 24 Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. 25 Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe? 26 Kwa sababu kila atakayenionea haya mimi na maneno yangu, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wake na wa Baba na wa malaika watakatifu. 27 Nami nawaambia kweli, Wapo katika hawa wanaosimama hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata wauone kwanza ufalme wa Mungu. 28 Baada ya maneno hayo yapata siku nane, aliwatwaa Petro na Yohana na Yakobo, akapanda mlimani ili kuomba. 29 Ikawa katika kusali kwake sura ya uso wake ikageuka, mavazi yake yakawa meupe, yakimeta-meta. 30 Na tazama, watu wawili walikuwa wakizungumza naye, nao ni Musa na Eliya; 31 walioonekana katika utukufu, wakanena habari za kufariki kwake atakakotimiza Yerusalemu. 32 Petro na wale waliokuwa pamoja naye walikuwa wamelemewa na usingizi; lakini walipokwisha amka waliuona utukufu wake, na wale wawili waliosimama pamoja naye. 33 Ikawa hao walipokuwa wakijitenga naye, Petro alimwambia Yesu, Bwana mkubwa, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu; kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya; hali hajui asemalo. 34 Alipokuwa akisema hayo, lilitokea wingu likawatia uvuli, wakaogopa walipoingia katika wingu hilo. 35 Sauti ikatoka katika wingu, ikisema, Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye. 36 Na sauti hiyo ilipokwisha, Yesu alionekana yu peke yake. Nao wakanyamaza, wasitangaze kwa mtu siku zile lo lote katika hayo waliyoyaona. 37 Ikawa siku ya pili yake, waliposhuka mlimani, mkutano mkubwa ulikutana naye. 38 Na tazama, mtu mmoja katika mkutano alipaza sauti, akisema, Mwalimu, nakuomba umwangalie mwanangu; kwa kuwa yeye ni mwanangu pekee. 39 Na tazama, pepo humpagaa, naye mara hupiga kelele; tena humtia kifafa, huku anatokwa na povu, wala hamwachi ila kwa shida, akimchubua-chubua. 40 Nikawasihi wanafunzi wako wamtoe, wasiweze. 41 Yesu akajibu akasema, Enyi kizazi kisicho na imani, kilichopotoka, nitakaa nanyi na kuwachukulia hata lini? Mlete mwanao hapa. 42 Alipokuwa katika kumwendea, pepo akambwaga chini, akamtia kifafa. Yesu akamkemea pepo mchafu, akamponya mtoto, akamrudishia babaye. 43 Wote wakashangaa, wakiuona ukuu wa Mungu. Nao walipokuwa wakiyastaajabia mambo yote aliyoyafanya, aliwaambia wanafunzi wake, 44 Yashikeni maneno haya masikioni mwenu, kwa kuwa Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu. 45 Lakini hawakulifahamu neno lile, likafichwa kwao wasilitambue; wakaogopa kumwuliza maana yake neno lile. 46 Wakaanza kuhojiana, ni nani atakayekuwa mkubwa miongoni mwao. 47 Naye Yesu alipotambua mawazo ya mioyo yao, alitwaa mtoto mdogo akamweka karibu naye, 48 akawaambia, Ye yote atakayempokea mtoto huyu kwa jina langu anipokea mimi; na ye yote atakayenipokea mimi ampokea yeye aliyenituma. Kwa kuwa aliye mdogo miongoni mwenu nyote huyo ndiye mkubwa. 49 Yohana akajibu akamwambia; Bwana mkubwa, tuliona mtu anatoa pepo kwa jina lako; tukamkataza, kwa sababu hafuatani na sisi. 50 Yesu akamwambia, Msimkataze, kwa kuwa yeye ambaye si kinyume chenu yu upande wenu. 51 Ikawa, siku za kupaa kwake zilipokuwa karibu kutimia, yeye aliukaza uso wake kwenda Yerusalemu; 52 akatuma wajumbe kutangulia mbele ya uso wake; wakaenda wakaingia katika kijiji cha Wasamaria, ili kumtengenezea mahali. 53 Lakini wenyeji hawakumkaribisha kwa vile alivyouelekeza uso wake kwenda Yerusalemu. 54 Wanafunzi wake Yakobo na Yohana walipoona hayo, walisema, Bwana, wataka tuagize moto ushuke kutoka mbinguni, uwaangamize; kama Eliya naye alivyofanya? 55 Akawageukia, akawakanya. Akasema, Hamjui ni roho ya namna gani mliyo nayo. 56 Kwa maana Mwana wa Adamu hakuja kuziangamiza roho za watu, bali kuziokoa. Wakaondoka wakaenda mpaka kijiji kingine. 57 Nao walipokuwa wakienda njiani, mtu mmoja alimwambia, Nitakufuata ko kote utakakokwenda. 58 Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake. 59 Akamwambia mwingine, Nifuate. Akasema, Bwana, nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu. 60 Akamwambia Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu. 61 Mtu mwingine pia akamwambia, Bwana, nitakufuata; lakini, nipe ruhusa kwanza nikawaage watu wa nyumbani mwangu. 62 Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.

Luka 10

1 Basi, baada ya hayo Bwana aliweka na wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. 2 Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. 3 Enendeni, angalieni, nawatuma kama wana kondoo kati ya mbwa-mwitu. 4 Msichukue mfuko, wala mkoba, wala viatu; wala msimwamkie mtu njiani. 5 Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu; 6 na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu. 7 Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii. 8 Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; 9 waponyeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia. 10 Na mji wo wote mtakaouingia, nao hawawakaribishi, tokeni humo, nanyi mkipita katika njia zake semeni, 11 Hata mavumbi ya mji wenu yaliyogandamana na miguu yetu tunayakung'uta juu yenu. Lakini jueni hili, ya kuwa Ufalme wa Mungu umekaribia. 12 Nawaambia ya kwamba siku ile itakuwa rahisi zaidi Sodoma kuistahimili adhabu yake kuliko mji huo. 13 Ole wako Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza hiyo iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu tangu hapo, huku wakiketi katika nguo za kigunia na majivu. 14 Lakini, siku ya hukumu itakuwa rahisi Tiro na Sidoni kustahimili adhabu zake kuliko ninyi. 15 Nawe Kapernaumu, je! Utakuzwa hata mbinguni? Utashushwa hata kuzimu. 16 Awasikilizaye ninyi anisikiliza mimi, naye awakataaye ninyi anikataa mimi; naye anikataaye mimi amkataa yeye aliyenituma. 17 Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha, wakisema, Bwana, hata pepo wanatutii kwa jina lako. 18 Akawaambia, Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni kama umeme. 19 Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru. 20 Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii; bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni. 21 Saa ile ile alishangilia kwa Roho Mtakatifu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza. 22 Akasema, Nimekabidhiwa vyote na Baba yangu, wala hakuna amjuaye Mwana ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia. 23 Akawageukia wanafunzi wake, akasema nao kwa faragha, Heri macho yaonayo mnayoyaona ninyi. 24 Kwa kuwa nawaambia ya kwamba manabii wengi na wafalme walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi wasiyasikie. 25 Na tazama, mwana-sheria mmoja alisimama amjaribu; akisema, Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele? 26 Akamwambia, Imeandikwa nini katika torati? Wasomaje? 27 Akajibu akasema, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako. 28 Akamwambia, Umejibu vema; fanya hivi nawe utaishi. 29 Naye akitaka kujidai haki, alimwuliza Yesu, Na jirani yangu ni nani? 30 Yesu akajibu akasema, Mtu mmoja alishuka toka Yerusalemu kwenda Yeriko, akaangukia kati ya wanyang'anyi; wakamvua nguo, wakamtia jeraha, wakaenda zao, wakimwacha karibu ya kufa. 31 Kwa nasibu kuhani mmoja alishuka kwa njia ile; na alipomwona alipita kando. 32 Na Mlawi vivyo hivyo, alipofika pale akamwona, akapita kando. 33 Lakini, Msamaria mmoja katika kusafiri kwake alifika hapo alipo; na alipomwona alimhurumia, 34 akakaribia, akamfunga jeraha zake, akizitia mafuta na divai; akampandisha juu ya mnyama wake, akampeleka mpaka nyumba ya wageni, akamtunza. 35 Hata siku ya pili akatoa dinari mbili, akampa mwenye nyumba ya wageni, akisema, Mtunze huyu, na cho chote utakachogharimiwa zaidi, mimi nitakaporudi nitakulipa. 36 Waonaje wewe, katika hao watatu, ni yupi aliyekuwa jirani yake yule aliyeangukia kati ya wanyang'anyi? 37 Akasema, Ni huyo aliyemwonea huruma. Yesu akamwambia, Enenda zako, nawe ukafanye vivyo hivyo. 38 Ikawa katika kuenenda kwao aliingia katika kijiji kimoja; mwanamke mmoja jina lake Martha akamkaribisha nyumbani kwake. 39 Naye alikuwa na umbu lake aitwaye Mariamu, aliyeketi miguuni pake Yesu, akasikiliza maneno yake. 40 Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. 41 Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; 42 lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa.

Luka 11

1 Ikawa alipokuwa mahali fulani akiomba, alipokwisha, mmoja katika wanafunzi wake alimwambia, Bwana, tufundishe sisi kusali, kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake. 2 Akawaambia, Msalipo, semeni, Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni. 3 Utupe siku kwa siku riziki yetu. 4 Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni lakini tuokoe na yule mwovu. 5 Akawaambia, Ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, Rafiki yangu, nikopeshe mikate mitatu, 6 kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, nami sina kitu cha kuweka mbele yake; 7 na yule wa ndani amjibu akisema, Usinitaabishe; mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe? 8 Nawaambia ya kwamba, ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake. 9 Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. 10 Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. 11 Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? 12 Au akimwomba yai, atampa nge? 13 Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao? 14 Naye alikuwa akitoa pepo bubu; ikawa pepo alipotoka, yule bubu akanena, makutano wakastaajabu. 15 Wengine wao wakasema, Atoa pepo kwa Beelzebuli, mkuu wa pepo. 16 Wengine walimjaribu, wakimtaka ishara itokayo mbinguni. 17 Naye akajua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya nyumba huanguka. 18 Basi, ikiwa Shetani naye amefitinika juu ya nafsi yake, ufalme wake utasimamaje? Kwa kuwa ninyi mnasema kwamba mimi natoa pepo kwa Beelzebuli. 19 Basi, kama mimi nikitoa pepo kwa Beelzebuli, wana wenu je! Huwatoa kwa nani? Kwa sababu hiyo, hao ndio watakaowahukumu. 20 Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia. 21 Mtu mwenye nguvu aliyejifunga silaha zake, alindapo nyumba yake, vitu vyake vi salama; 22 lakini mtu mwenye nguvu kuliko yeye atakapomwendea na kumshinda, amnyang'anya silaha zake zote alizokuwa akizitegemea, na kuyagawanya mateka yake. 23 Mtu ambaye si pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya. 24 Pepo mchafu amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika; asipoona, husema, 25 Nitairudia nyumba yangu niliyotoka. 26 Hata afikapo, akaiona imefagiwa na kupambwa, ndipo huenda akachukua pepo wengine saba, walio waovu kuliko yeye mwenyewe, wakaingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza. 27 Ikawa alipokuwa akisema maneno hayo, mwanamke mmoja katika mkutano alipaza sauti yake, akamwambia, Heri tumbo lililokuzaa, na matiti uliyonyonya. 28 Lakini yeye alisema, Afadhali, heri walisikiao neno la Mungu na kulishika. 29 Na makutano walipokuwa wakimkusanyikia, alianza kusema, Kizazi hiki ni kizazi kibaya; kinatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya Yona. 30 Maana, kama vile Yona alivyokuwa ishara kwa Waninawi, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu kwa kizazi hiki. 31 Malkia wa Kusini ataondoka siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa na hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka ncha za dunia aisikie hekima ya Sulemani; na hapa pana mkubwa kuliko Sulemani. 32 Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na kizazi hiki, nao watakihukumu kuwa na hatia; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona, na hapa pana mkubwa kuliko Yona. 33 Hakuna mtu awashaye taa na kuiweka mahali palipositirika, au chini ya pishi; bali huiweka juu ya kiango, ili waingiao wapate kuuona mwanga. 34 Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote unao mwanga; lakini likiwa bovu, mwili wako nao una giza. 35 Angalia basi, mwanga ulio ndani yako usije ukawa giza. 36 Basi kama mwanga umeenea katika mwili wako wote, wala hauna sehemu iliyo na giza, mwili wako wote utakuwa na mwanga mtupu; kama vile taa ikumulikiapo kwa mwanga wake. 37 Alipokuwa akinena, Farisayo mmoja alimwita aje kwake ale chakula; akaingia, akaketi chakulani. 38 Farisayo huyo alipomwona, alistaajabu kwa sababu hakunawa kabla ya chakula. 39 Bwana akamwambia, Ninyi Mafarisayo mwasafisha kikombe na sahani kwa nje, lakini ndani yenu mmejaa unyang'anyi na uovu. 40 Enyi wapumbavu; aliyevifanya vya nje, siye yeye aliyevifanya vya ndani pia? 41 Lakini, toeni sadaka vile vya ndani, na tazama, vyote huwa safi kwenu. 42 Lakini, ole wenu, Mafarisayo, kwa kuwa mwatoa zaka za mnanaa na mchicha na kila mboga, na huku mwaacha mambo ya adili, na upendo wa Mungu; iliwapasa kuyafanya hayo ya kwanza, bila kuyaacha hayo ya pili. 43 Ole wenu, Mafarisayo, kwa kuwa mwapenda kuketi mbele katika masinagogi, na kusalimiwa masokoni. 44 Ole wenu, kwa kuwa mmefanana na makaburi yasiyoonekana, ambayo watu wapitao juu yake hawana habari nayo. 45 Mtu mmoja katika wana-sheria akajibu, akamwambia, Mwalimu, kwa kusema hayo umetushutumu sisi nasi. 46 Akasema, Nanyi wana-sheria, ole wenu, kwa sababu mwawatwika watu mizigo isiyochukulika, wala ninyi wenyewe hamwigusi mizigo hiyo hata kwa kimoja cha vidole vyenu. 47 Ole wenu, kwa kuwa mwajenga maziara ya manabii, na baba zenu ndio waliowaua. 48 Basi, mwashuhudia na kuziridhia kazi za baba zenu; kwa kuwa wao waliwaua nanyi mwawajengea maziara. 49 Na kwa sababu hiyo hekima ya Mungu ilisema, Tazama, nitatuma kwao manabii na mitume, nao watawaua baadhi yao na kuwafukuza, 50 ili kwa kizazi hiki itakwe damu ya manabii wote, iliyomwagika tangu kupigwa msingi wa ulimwengu; 51 tangu damu ya Habili hata damu ya Zakaria, aliyeuawa kati ya madhabahu na hekalu. Naam, nawaambieni ya kwamba itatakwa kwa kizazi hiki. 52 Ole wenu, enyi wana-sheria, kwa kuwa mmeuondoa ufunguo wa maarifa; wenyewe hamkuingia, na wale waliokuwa wakiingia mmewazuia. 53 Alipotoka humo, waandishi na Mafarisayo walianza kumsonga vibaya, na kumchokoza kwa maswali mengi, 54 wakimvizia, ili wapate neno litokalo kinywani mwake.

Luka 12

1 Wakati huo, makutano walipokutanika elfu elfu, hata wakakanyagana, alianza kuwaambia wanafunzi wake kwanza, Jilindeni na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki. 2 Lakini hakuna neno lililositirika ambalo halitafunuliwa, wala lililofichwa ambalo halitajulikana. 3 Basi, yo yote mliyosema gizani yatasikiwa mwangani; na mliyonena sikioni mwa mtu katika vyumba vya ndani, yatahubiriwa juu ya dari. 4 Nami nawaambia ninyi rafiki zangu, msiwaogope hao wauuao mwili, kisha baada ya hayo hawana wawezalo kutenda zaidi. 5 Lakini nitawaonya mtakayemwogopa; mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo. 6 Je! Mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? Wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. 7 Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi. 8 Nami nawaambia, kila atakayenikiri mbele ya watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika wa Mungu; 9 na mwenye kunikana mbele ya watu, huyo atakanwa mbele ya malaika wa Mungu. 10 Na kila mtu atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali aliyemkufuru Roho Mtakatifu hatasamehewa. 11 Na watakapowapeleka ninyi mbele ya masinagogi na maliwali na wenye mamlaka, msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; 12 kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema. 13 Mtu mmoja katika mkutano akamwambia, Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi wetu. 14 Akamwambia, Mtu wewe, ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu? 15 Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo. 16 Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; 17 akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. 18 Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. 19 Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. 20 Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? 21 Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu. 22 Akawaambia wanafunzi wake, Kwa sababu hiyo nawaambia, Msisumbukie maisha yenu, mtakula nini; wala miili yenu, mtavaa nini. 23 Kwa kuwa maisha ni zaidi ya chakula, na mwili ni zaidi ya mavazi. 24 Watafakarini kunguru, ya kwamba hawapandi wala hawavuni; hawana ghala wala uchaga, na Mungu huwalisha. Bora ninyi mara nyingi kuliko ndege! 25 Na yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? 26 Basi, ikiwa hamwezi hata neno lililo dogo, kwa nini kujisumbua kwa ajili ya yale mengine? 27 Yatafakarini maua jinsi yameavyo; hayatendi kazi wala hayasokoti; nami nawaambia ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. 28 Basi, ikiwa Mungu huvika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatawatendea ninyi zaidi, enyi wa imani haba? 29 Ninyi msitafute mtakavyokula wala mtakavyokunywa; wala msifanye wasiwasi, 30 kwa maana, hayo yote ndiyo watafutayo mataifa ya duniani, lakini Baba yenu anajua ya kuwa mna haja na hayo. 31 Bali utafuteni ufalme wa Mungu, na hayo mtaongezewa. 32 Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme. 33 Viuzeni mlivyo navyo, mtoe sadaka. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, akiba isiyopungua katika mbingu, mahali pasipokaribia mwivi, wala nondo haharibu. 34 Kwa kuwa hazina yenu ilipo, ndipo itakapokuwapo na mioyo yenu. 35 Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka; 36 nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao, atakaporudi kutoka arusini, ili atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara. 37 Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha. Amin, nawaambieni, atajifunga na kuwakaribisha chakulani, atakuja na kuwahudumia. 38 Na akija zamu ya pili, au akija zamu ya tatu, na kuwakuta hivi, heri watumwa hao. 39 Lakini fahamuni neno hili, Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa. 40 Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu. 41 Petro akamwambia, Bwana, mithali hiyo umetuambia sisi tu, au watu wote pia? 42 Bwana akasema, Ni nani, basi, aliye wakili mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya utumishi wake wote, awape watu posho kwa wakati wake? 43 Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta anafanya hivyo. 44 Kweli nawaambia, atamweka juu ya vitu vyake vyote. 45 Lakini, mtumwa yule akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia kuja, akaanza kuwapiga wajoli wake, wanaume kwa wanawake, akila na kunywa na kulewa; 46 bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wasioamini. 47 Na mtumwa yule aliyejua mapenzi ya bwana wake, asijiweke tayari, wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa sana. 48 Na yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi. 49 Nimekuja kutupa moto duniani; na ukiwa umekwisha washwa, ni nini nitakalo zaidi? 50 Lakini nina ubatizo unipasao kubatiziwa, nami nina dhiki kama nini hata utimizwe! 51 Je! Mwadhani ya kwamba nimekuja kuleta amani duniani? Nawaambia, La, sivyo, bali mafarakano. 52 Kwa kuwa tokea sasa katika nyumba moja watakuwamo watu watano wamefarakana, watatu kwa wawili, wawili kwa watatu. 53 Watafarakana baba na mwanawe, na mwana na babaye; mama na binti yake, na binti na mamaye; mkwe mtu na mkwewe, mkwe na mkwe mtu. 54 Akawaambia makutano pia, Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo. 55 Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo. 56 Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya? 57 Na mbona ninyi wenyewe kwa nafsi zenu hamwamui yaliyo haki? 58 Maana, unapofuatana na mshitaki wako kwenda kwa mwamuzi, hapo njiani fanya bidii kupatanishwa naye, asije akakuburuta mpaka mbele ya kadhi; yule kadhi akakutia mikononi mwake mwenye kulipiza, na yule mwenye kulipiza akakutupa gerezani. 59 Nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.

Luka 13

1 Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichanganya damu yao na dhabihu zao. 2 Akawajibu akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? 3 Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. 4 Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamba wao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? 5 Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. 6 Akanena mfano huu; Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate. 7 Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu? 8 Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; 9 nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate. 10 Siku ya sabato alikuwa akifundisha katika sinagogi mojawapo. 11 Na tazama, palikuwa na mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa. 12 Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako. 13 Akaweka mikono yake juu yake, naye akanyoka mara hiyo, akamtukuza Mungu. 14 Basi mkuu wa sinagogi alikasirika kwa sababu Yesu amemponya mtu siku ya sabato, akajibu, akawaambia mkutano, Kuna siku sita zifaazo kufanya kazi, basi njoni mponywe katika siku hizo, wala si katika siku ya sabato. 15 Lakini Bwana akajibu akasema, Enyi wanafiki, kila mmoja wenu, je! Hamfungui ng'ombe wake au punda wake siku ya sabato katika zizi, aende naye kumnywesha? 16 Na huyu mwanamke, aliye wa uzao wa Ibrahimu, ambaye Shetani amemfunga miaka kumi na minane hii, haikupasa afunguliwe kifungo hiki siku ya sabato? 17 Aliposema haya wakatahayari wote walioshindana naye; mkutano wote wakafurahi kwa sababu ya mambo matukufu yaliyotendwa na yeye. 18 Kisha alisema, Ufalme wa Mungu umefanana na nini? Nami niufananishe na nini? 19 Umefanana na punje ya haradali aliyotwaa mtu akaitupa katika shamba lake; ikamea, ikawa mti; ndege wa angani wakakaa katika matawi yake. 20 Akasema mara ya pili, Niufananishe na nini ufalme wa Mungu? 21 Umefanana na chachu aliyotwaa mwanamke akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachacha wote pia. 22 Naye alikuwa akipita katika miji na vijiji, akifundisha, katika safari yake kwenda Yerusalemu. 23 Mtu mmoja akamwuliza, Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache? Akawaambia, 24 Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze. 25 Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako; 26 ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu. 27 Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu. 28 Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje. 29 Nao watakuja watu toka mashariki na magharibi, na toka kaskazini na kusini, nao wataketi chakulani katika ufalme wa Mungu. 30 Na tazama, wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa mwisho. 31 Saa ile ile Mafarisayo kadha wa kadha walimwendea, wakamwambia, Toka hapa, uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua. 32 Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika. 33 Pamoja na hayo imenipasa kushika njia yangu leo na kesho na kesho kutwa; kwa kuwa haimkini nabii aangamie nje ya Yerusalemu. 34 Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii na kuwapiga kwa mawe waliotumwa kwako, mara ngapi nimetaka kuwakusanya watoto wako kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake chini ya mbawa zake, wala hamkutaka. 35 Angalieni, mmeachiwa nyumba yenu! Nami nawaambia, Hamtaniona tena kamwe, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana.

Luka 14

1 Ikawa alipoingia ndani ya nyumba ya mtu mmoja miongoni mwa wakuu wa Mafarisayo siku ya sabato, ale chakula, walikuwa wakimvizia. 2 Na tazama, mbele yake palikuwa na mtu mwenye ugonjwa wa safura. 3 Yesu akajibu, akawaambia wana-sheria na Mafarisayo, Je! Ni halali kuponya siku ya sabato, ama sivyo? 4 Wao wakanyamaza. Akamshika, akamponya, akamruhusu aende zake. 5 Akawaambia, Ni nani miongoni mwenu, ikiwa ng'ombe wake au punda wake ametumbukia kisimani, asiyemwopoa mara hiyo siku ya sabato? 6 Nao hawakuweza kujibu maneno haya. 7 Akawaambia mfano wale walioalikwa, alipoona jinsi walivyochagua viti vya mbele; akisema, 8 Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, 9 akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma. 10 Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe. 11 Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa. 12 Akamwambia na yule aliyemwalika, Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo. 13 Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, 14 nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki. 15 Basi aliposikia hayo mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja naye alimwambia, Heri yule atakayekula mkate katika ufalme wa Mungu. 16 Akamwambia, Mtu mmoja alifanya karamu kubwa akaalika watu wengi, 17 akamtuma mtumwa wake saa ya chakula awaambie wale walioalikwa, Njoni, kwa kuwa vitu vyote vimekwisha kuwekwa tayari. 18 Wakaanza wote kutoa udhuru kwa nia moja. Wa kwanza alimwambia, Nimenunua shamba, sharti niende nikalitazame; tafadhali unisamehe. 19 Mwingine akasema, Nimenunua ng'ombe jozi tano, ninakwenda kuwajaribu; tafadhali unisamehe. 20 Mwingine akasema, Nimeoa mke, na kwa sababu hiyo siwezi kuja. 21 Yule mtumwa akaenda, akampa bwana wake habari ya mambo hayo. Basi, yule mwenye nyumba akakasirika, akamwambia mtumwa wake, Toka upesi, uende katika njia kuu na vichochoro vya mji, ukawalete hapa maskini, na vilema, na vipofu, na viwete. 22 Mtumwa akasema, Bwana, hayo uliyoagiza yamekwisha tendeka, na hata sasa ingaliko nafasi. 23 Bwana akamwambia mtumwa, Toka nje uende barabarani na mipakani, ukawashurutishe kuingia ndani, nyumba yangu ipate kujaa. 24 Maana nawaambia ya kwamba katika wale walioalikwa, hapana hata mmoja atakayeionja karamu yangu. 25 Makutano mengi walipokuwa wakifuatana naye, aligeuka, akawaambia, 26 Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu. 27 Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu. 28 Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia? 29 Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi, watu wote waonao wakaanza kumdhihaki, 30 wakisema, Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza. 31 Au kuna mfalme gani, akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana na yule anayekuja juu yake na watu elfu ishirini? 32 Na kama akiona hawezi, hutuma ujumbe kutaka sharti za amani, mtu yule akali mbali. 33 Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu. 34 Chumvi ni kitu chema; lakini chumvi ikiwa imeharibika, itiwe nini ikolee? 35 Haiifai nchi wala jaa; watu huitupa nje. Mwenye masikio ya kusikilia, na asikie.

Luka 15

1 Basi watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia wamsikilize. 2 Mafarisayo na waandishi wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao. 3 Akawaambia mfano huu, akisema, 4 Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone? 5 Naye akiisha kumwona, humweka mabegani pake akifurahi. 6 Na afikapo nyumbani kwake, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimekwisha kumpata kondoo wangu aliyepotea. 7 Nawaambia, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu. 8 Au kuna mwanamke gani mwenye shilingi kumi, akipotewa na moja, asiyewasha taa na kufagia nyumba, na kutafuta kwa bidii hata aione? 9 Na akiisha kuiona, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimeipata tena shilingi ile iliyonipotea. 10 Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye. 11 Akasema, Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; 12 yule mdogo akamwambia babaye, Baba, nipe sehemu ya mali inayoniangukia. Akawagawia vitu vyake. 13 Hata baada ya siku si nyingi, yule mdogo akakusanya vyote, akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati. 14 Alipokuwa amekwisha tumia vyote, njaa kuu iliingia nchi ile, yeye naye akaanza kuhitaji. 15 Akaenda akashikamana na mwenyeji mmoja wa nchi ile; naye alimpeleka shambani kwake kulisha nguruwe. 16 Akawa akitamani kujishibisha kwa maganda waliyokula nguruwe, wala hapana mtu aliyempa kitu. 17 Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. 18 Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; 19 sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako. 20 Akaondoka, akaenda kwa babaye. Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana. 21 Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena. 22 Lakini baba aliwaambia watumwa wake, Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; 23 mleteni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; 24 kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia. 25 Basi, yule mwanawe mkubwa alikuwako shamba na alipokuwa akija na kuikaribia nyumba, alisikia sauti ya nyimbo na machezo. 26 Akaita mtumishi mmoja, akamwuliza, Mambo haya, maana yake nini? 27 Akamwambia, Ndugu yako amekuja, na baba yako amemchinja ndama aliyenona, kwa sababu amempata tena, yu mzima. 28 Akakasirika, akakataa kuingia ndani. Basi babaye alitoka nje, akamsihi. 29 Akamjibu baba yake, akasema, Tazama, mimi nimekutumikia miaka mingapi hii, wala sijakosa amri yako wakati wo wote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nifanye furaha na rafiki zangu; 30 lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona. 31 Akamwambia, Mwanangu, wewe u pamoja nami sikuzote, na vyote nilivyo navyo ni vyako. 32 Tena, kufanya furaha na shangwe ilipasa, kwa kuwa huyu ndugu yako alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana.

Luka 16

1 Tena, aliwaambia wanafunzi wake, Palikuwa na mtu mmoja, tajiri, aliyekuwa na wakili wake; huyu alishitakiwa kwake kuwa anatapanya mali zake. 2 Akamwita, akamwambia, Ni habari gani hii ninayosikia juu yako? Toa hesabu ya uwakili wako, kwa kuwa huwezi kuwa wakili tena. 3 Yule wakili akasema moyoni mwake, Nifanyeje? Maana, bwana wangu ananiondolea uwakili. Kulima, siwezi; kuomba, naona haya. 4 Najua nitakalotenda, ili nitakapotolewa katika uwakili, wanikaribishe nyumbani mwao. 5 Akawaita wadeni wa bwana wake, kila mmoja; akamwambia wa kwanza, Wawiwani na bwana wangu? 6 Akasema, Vipimo mia vya mafuta. Akamwambia, Twaa hati yako, keti upesi, andika hamsini. 7 Kisha akamwambia mwingine, Na wewe wawiwani? Akasema, Makanda mia ya ngano. Akamwambia, Twaa hati yako, andika themanini. 8 Yule bwana akamsifu wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa busara; kwa kuwa wana wa ulimwengu huu katika kizazi chao wenyewe huwa na busara kuliko wana wa nuru. 9 Nami nawaambia, Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu, ili itakapokosekana wawakaribishe katika makao ya milele. 10 Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia. 11 Basi, kama ninyi hamkuwa waaminifu katika mali ya udhalimu, ni nani atakayewapa amana mali ya kweli? 12 Na kama hamkuwa waaminifu katika mali ya mtu mwingine, ni nani atakayewapa iliyo yenu wenyewe? 13 Hakuna mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia huyu na kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali. 14 Basi Mafarisayo, ambao wenyewe ni wapenda fedha, waliyasikia hayo yote, wakamdhihaki. 15 Akawaambia, Ninyi ndinyi mnaojidai haki mbele ya wanadamu, lakini Mungu awajua mioyo yenu; kwa kuwa lililotukuka kwa wanadamu huwa chukizo mbele za Mungu. 16 Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu. 17 Lakini ni vyepesi zaidi mbingu na nchi vitoweke, kuliko itanguke nukta moja ya torati. 18 Kila amwachaye mkewe na kumwoa mke mwingine azini; naye amwoaye yeye aliyeachwa na mumewe azini. 19 Akasema, Palikuwa na mtu mmoja, tajiri, aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, na kula sikuzote kwa anasa. 20 Na maskini mmoja, jina lake Lazaro, huwekwa mlangoni pake, ana vidonda vingi, 21 naye alikuwa akitamani kushibishwa kwa makombo yaliyoanguka katika meza ya yule tajiri; hata mbwa wakaja wakamramba vidonda vyake. 22 Ikawa yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa. 23 Basi, kule kuzimu aliyainua macho yake, alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake. 24 Akalia, akasema, Ee baba Ibrahimu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu. 25 Ibrahimu akasema, Mwanangu, kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa. 26 Na zaidi ya hayo, kati yetu sisi na ninyi kumewekwa shimo kubwa, ili wale watakao kutoka huku kwenda kwenu wasiweze; wala watu wa kwenu wasivuke kuja kwetu. 27 Akasema, Basi, baba, nakuomba, umtume nyumbani kwa baba yangu, 28 kwa kuwa ninao ndugu watano, ili awashuhudie, wasije wao pia wakafika mahali hapa pa mateso. 29 Ibrahimu akasema, Wanao Musa na manabii; na wawasikilize wao. 30 Akasema, La, baba Ibrahimu, lakini kama akiwaendea mtu atokaye kwa wafu, watatubu. 31 Akamwambia, Wasipowasikia Musa na manabii, hawatashawishwa hata mtu akifufuka katika wafu.

Luka 17

1 Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! 2 Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa. 3 Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe. 4 Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe. 5 Mitume wakamwambia Bwana, Tuongezee imani. 6 Bwana akasema, Kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng'oka, ukapandwe baharini, nao ungewatii. 7 Lakini, ni nani kwenu mwenye mtumwa alimaye au achungaye ng'ombe, atakayemwambia mara arudipo kutoka shambani, Njoo upesi, keti, ule chakula? 8 Je! Hatamwambia, Nifanyie tayari chakula, nile; jifunge unitumikie, hata niishe kula na kunywa, ndipo nawe utakapokula na kunywa? 9 Je! Atampa asante yule mtumwa, kwa sababu ameyafanya aliyoagizwa? 10 Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya. 11 Ikawa walipokuwa njiani kwenda Yerusalemu, alikuwa akipita katikati ya Samaria na Galilaya. 12 Na alipoingia katika kijiji kimoja, alikutana na watu kumi wenye ukoma; wakasimama mbali, 13 wakapaza sauti wakisema, Ee Yesu, Bwana mkubwa, uturehemu! 14 Alipowaona aliwaambia, Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani. Ikawa walipokuwa wakienda walitakasika. 15 Na mmoja wao alipoona kwamba amepona, alirudi, huku akimtukuza Mungu kwa sauti kuu; 16 akaanguka kifudifudi miguuni pake, akamshukuru; naye alikuwa Msamaria. 17 Yesu akajibu, akanena, Hawakutakaswa wote kumi? Wale kenda wa wapi? 18 Je! Hawakuonekana waliorudi kumpa Mungu utukufu ila mgeni huyu? 19 Akamwambia, Inuka, enenda zako, imani yako imekuokoa. 20 Na alipoulizwa na Mafarisayo, Ufalme wa Mungu utakuja lini? Aliwajibu akawaambia, ufalme wa Mungu hauji kwa kuuchunguza; 21 wala hawatasema, Tazama, upo huku, au, kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo ndani yenu. 22 Akawaambia wanafunzi, Siku zitakuja mtakapotamani kuona siku moja katika siku zake Mwana wa Adamu, msiione. 23 Tena watawaambia, Tazama, kule! Tazama, huku! Msiondoke mahali mlipo, wala msiwafuate; 24 kwa kuwa, kama vile umeme umulikavyo toka upande huu chini ya mbingu hata upande huu chini ya mbingu, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu katika siku yake. 25 Lakini kwanza, hana budi kupata mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki. 26 Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika siku zake Mwana wa Adamu. 27 Walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakioa na kuolewa, hata siku ile Nuhu aliyoingia katika safina, gharika ikashuka ikawaangamiza wote. 28 Na kadhalika, kama ilivyokuwa katika siku za Lutu, walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakinunua na kuuza, wakipanda na kujenga; 29 lakini siku ile Lutu aliyotoka Sodoma kulinyesha moto na kibiriti kutoka mbinguni vikawaangamiza wote. 30 Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu. 31 Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma. 32 Mkumbukeni mkewe Lutu. 33 Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya. 34 Nawaambia, usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. 35 Wanawake wawili watakuwa wakisaga pamoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. 36 Watu wawili watakuwa shambani, mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. 37 Wakajibu, wakamwuliza, Wapi, Bwana? Akawaambia, Ulipo mzoga, ndipo watakapokutanika tai.

Luka 18

1 Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. 2 Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. 3 Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. 4 Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, 5 lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima. 6 Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. 7 Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? 8 Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani? 9 Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. 10 Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. 11 Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. 12 Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. 13 Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. 14 Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa. 15 Wakamletea na watoto wachanga ili awaguse; lakini wanafunzi walipoona waliwakemea. 16 Bali Yesu akawaita waje kwake, akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu, wala msiwazuie, kwa kuwa watu kama hao ufalme wa Mungu ni wao. 17 Amin, nawaambia, Mtu ye yote asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hauingii kamwe. 18 Tena, mtu mkubwa mmoja alimwuliza, akisema, Mwalimu mwema, nifanye nini ili nipate kuurithi uzima wa milele? 19 Yesu akamwambia, Mbona unaniita mwema? Hakuna aliye mwema ila mmoja, naye ndiye Mungu. 20 Wazijua amri; Usizini, Usiue, Usiibe, Usishuhudie uongo, Waheshimu baba yako na mama yako. 21 Akasema, Hayo yote nimeyashika tangu utoto wangu. 22 Yesu aliposikia hayo alimwambia, Umepungukiwa na neno moja bado; viuze ulivyo navyo vyote, ukawagawanyie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha, njoo unifuate. 23 Lakini aliposikia hayo alihuzunika sana, maana alikuwa na mali nyingi. 24 Yesu alipoona vile alisema, Kwa shida gani wenye mali watauingia ufalme wa Mungu! 25 Kwa maana ni vyepesi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu. 26 Nao waliosikia walisema, Ni nani basi awezaye kuokoka? 27 Akasema, Yasiyowezekana kwa wanadamu yawezekana kwa Mungu. 28 Petro akasema, Tazama, sisi tumeviacha vitu vyetu vyote na kukufuata. 29 Akawaambia, Hakika nawaambia, hakuna mtu aliyeacha nyumba, au mke, au ndugu, au wazazi, au wana, kwa ajili ya ufalme wa Mungu, 30 asiyepokea zaidi mara nyingi katika zamani hizi, na katika ulimwengu ujao uzima wa milele. 31 Akawachukua wale Thenashara, akawaambia, Tazameni, tunapanda kwenda Yerusalemu, na mambo yote yatatimizwa, Mwana wa Adamu aliyoandikiwa na manabii. 32 Kwa kuwa atatiwa mikononi mwa Mataifa, atafanyiwa dhihaka; atatendwa jeuri, na kutemewa mate; 33 nao watampiga mijeledi, kisha watamwua; na siku ya tatu atafufuka. 34 Walakini hawakuelewa maneno hayo hata kidogo, na jambo hilo lilikuwa limefichwa kwao, wala hawakufahamu yaliyonenwa. 35 Ikawa alipokaribia Yeriko, mtu mmoja kipofu alikuwa ameketi kando ya njia, akiomba sadaka; 36 na alipowasikia makutano wakipita, aliuliza, Kuna nini? 37 Wakamwambia, Yesu wa Nazareti anapita. 38 Akapiga kelele, akisema, Yesu, Mwana wa Daudi, unirehemu. 39 Basi wale waliotangulia wakamkemea ili anyamaze; lakini yeye alizidi sana kupaza sauti, Ee Mwana wa Daudi, unirehemu. 40 Yesu akasimama, akaamuru aletwe kwake; na alipomkaribia, alimwuliza, 41 Wataka nikufanyie nini? Akasema, Bwana, nipate kuona. 42 Yesu akamwambia, Upewe kuona; imani yako imekuponya. 43 Mara hiyo akapata kuona, akamfuata, huku akimtukuza Mungu. Na watu wote walipoona hayo walimsifu Mungu.

Luka 19

1 Naye alipoingia Yeriko alipita katikati yake. 2 Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. 3 Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. 4 Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile. 5 Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako. 6 Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. 7 Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi. 8 Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. 9 Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. 10 Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea. 11 Waliposikia hayo, aliongeza kusema mfano, kwa sababu alikuwa karibu na Yerusalemu, na wao walidhani ya kuwa ufalme wa Mungu utaonekana mara. 12 Basi akasema, Mtu mmoja, kabaila, alisafiri kwenda nchi ya mbali, ili ajipatie ufalme na kurudi. 13 Akaita watu kumi katika watumwa wake, akawapa mafungu kumi ya fedha, akawaambia, Fanyeni biashara hata nitakapokuja. 14 Lakini watu wa mji wake walimchukia, wakatuma wajumbe kumfuata na kusema, Hatumtaki huyu atutawale. 15 Ikawa aliporudi, ameupata ufalme wake, aliamuru waitwe wale watumwa aliowapa fedha, ili ajue faida aliyopata kila mtu kwa biashara yake. 16 Akaja wa kwanza, akasema, Bwana, fungu lako limeleta faida ya mafungu kumi zaidi. 17 Akamwambia, Vema, mtumwa mwema; kwa vile ulivyokuwa mwaminifu katika neno lililo dogo, uwe na mamlaka juu ya miji kumi. 18 Akaja wa pili, akasema, Bwana, fungu lako limeleta mafungu matano faida. 19 Akamwambia huyu naye, Wewe uwe juu ya miji mitano. 20 Akaja mwingine akasema, Bwana, hili ndilo fungu lako, ambalo nililiweka akiba katika leso. 21 Kwa maana nilikuogopa kwa kuwa u mtu mgumu; waondoa usichoweka, wavuna usichopanda. 22 Akamwambia, Nitakuhukumu kwa kinywa chako, mtumwa mwovu wewe. Ulinijua kuwa ni mtu mgumu, niondoaye nisichoweka, na kuvuna nisichopanda; 23 basi, mbona hukuiweka fedha yangu kwa watoao riba, ili nijapo niipate pamoja na faida yake? 24 Akawaambia waliosimama karibu, Mnyang'anyeni hilo fungu, mkampe yule mwenye mafungu kumi. 25 Wakamwambia, Bwana, anayo mafungu kumi. 26 Nawaambia, Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang'anywa hata alicho nacho. 27 Tena, wale adui zangu, wasiotaka niwatawale, waleteni hapa mwachinje mbele yangu. 28 Na alipokwisha kusema hayo, alitangulia mbele akipanda kwenda Yerusalemu. 29 Ikawa alipokaribia Bethfage na Bethania, kwenye mlima uitwao wa Mizeituni, alituma wawili katika wale wanafunzi, 30 akisema, Nendeni mpaka kijiji kile kinachowakabili, na mtakapoingia ndani mtaona mwana-punda, amefungwa, ambaye hajapandwa na mtu ye yote bado, mfungueni mkamlete hapa. 31 Na kama mtu akiwauliza, Mbona mnamfungua? Semeni hivi, Bwana anamhitaji. 32 Na wale waliotumwa wakaenda wakaona kama alivyowaambia. 33 Na walipokuwa wakimfungua mwana-punda, wenyewe waliwaambia, Mbona mnamfungua mwana-punda? 34 Wakasema, Bwana ana haja naye. 35 Wakampeleka kwa Yesu, wakatandika nguo zao juu ya mwana-punda, wakampandisha Yesu. 36 Na alipokuwa akienda walitandaza nguo zao njiani. 37 Hata alipokuwa amekaribia matelemko ya mlima wa Mizeituni, kundi zima la wanafunzi wake walianza kufurahi na kumsifu Mungu kwa sauti kuu, kwa ajili ya matendo yote ya uwezo waliyoyaona, 38 wakasema, Ndiye mbarikiwa Mfalme ajaye kwa jina la Bwana; amani mbinguni, na utukufu huko juu. 39 Baadhi ya Mafarisayo waliokuwa katika mkutano wakamwambia, Mwalimu, uwakanye wanafunzi wako. 40 Akajibu, akasema, Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele. 41 Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, 42 akisema, Laiti ungalijua, hata wewe katika siku hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. 43 Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; 44 watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua majira ya kujiliwa kwako. 45 Akaingia hekaluni, akaanza kuwatoa wale waliokuwa wakifanya biashara, 46 akiwaambia, Imeandikwa, Nyumba yangu itakuwa nyumba ya sala; lakini ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi. 47 Naye akawa akifundisha kila siku hekaluni. Lakini wakuu wa makuhani, na waandishi, na wakuu wa watu walikuwa wakitafuta njia ya kumwangamiza; 48 wasione la kutenda, kwa kuwa watu wote walikuwa wakiandamana naye, wakimsikiliza.

Luka 20

1 Ikawa siku moja, alipokuwa akiwafundisha watu hekaluni, na kuihubiri habari njema, wakuu wa makuhani na waandishi pamoja na wazee walimtokea ghafula; 2 wakamwambia, wakisema, Tuambie, unatenda mambo hayo kwa mamlaka gani? Tena, ni nani aliyekupa mamlaka hii? 3 Akajibu akawaambia, Nami nitawauliza ninyi neno moja; niambieni, 4 Ubatizo wa Yohana, je! Ulitoka mbinguni au kwa wanadamu? 5 Wakahojiana wao kwa wao, wakisema, Kama tukisema ulitoka mbinguni, atasema, Basi, mbona hamkumwamini? 6 Na tukisema ulitoka kwa wanadamu, watu wote watatupiga kwa mawe, kwa kuwa wamemkubali Yohana kuwa ni nabii. 7 Wakajibu, kwamba, Hatujui ulikotoka. 8 Yesu akawaambia, Wala mimi siwaambii ninyi ni kwa mamlaka gani ninatenda mambo haya. 9 Akaanza kuwaambia watu mfano huu; Mtu mmoja alipanda shamba la mizabibu; akapangisha wakulima, akaenda akakaa katika nchi nyingine muda mrefu. 10 Na wakati wa mavuno alituma mtumwa kwa wale wakulima ili wampe baadhi ya matunda ya mizabibu; wakulima wakampiga wakamfukuza mikono mitupu. 11 Akatuma na mtumwa mwingine. Wakampiga huyu naye, wakamwaibisha wakamfukuza mikono mitupu. 12 Akamtuma na wa tatu; huyu naye wakamtia jeraha, wakamtupa nje. 13 Basi, bwana wa shamba la mizabibu alisema, Nifanyeje? Nitamtuma mwanangu, mpendwa wangu; yamkini watamheshimu yeye. 14 Lakini, wale wakulima walipomwona, walishauriana wao kwa wao, wakisema, Huyu ndiye mrithi; haya, na tumwue, ili urithi uwe wetu. 15 Wakamtupa nje ya shamba la mizabibu, wakamwua. Basi, bwana wa shamba la mizabibu atawatendeje? 16 Atakuja na kuwaangamiza wakulima wale, na lile shamba la mizabibu atawapa wengine. Waliposikia hayo walisema, Hasha! Yasitukie haya! 17 Akawakazia macho akasema, Maana yake nini basi neno hili lililoandikwa, Jiwe walilolikataa waashi, Hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni? 18 Kila mtu aangukaye juu ya jiwe hilo atavunjika-vunjika; na ye yote ambaye litamwangukia litamsaga kabisa. 19 Nao waandishi na wakuu wa makuhani walitafuta kumkamata saa iyo hiyo, wakawaogopa watu, maana walitambua ya kwamba mfano huu amewanenea wao. 20 Wakamvizia-vizia, wakatuma wapelelezi waliojifanya kuwa watu wa haki, ili wamnase katika maneno yake, wapate kumtia katika enzi na mamlaka ya liwali. 21 Wakamwuliza, wakisema, Mwalimu, twajua ya kwamba wasema na kufundisha yaliyo ya haki, wala hujali cheo cha mtu, bali unafundisha njia ya Mungu kwa kweli. 22 Je! Ni halali tumpe Kaisari kodi, au sivyo? 23 Lakini yeye alitambua hila yao, akawaambia, 24 Nionyesheni dinari. Ina sura na anwani ya nani? Wakamjibu, Ya Kaisari. 25 Akawaambia, Basi, vya Kaisari mpeni Kaisari, na vya Mungu mpeni Mungu. 26 Wala hawakuweza kumshitaki kwa maneno yake mbele ya watu; wakastaajabia majibu yake, wakanyamaa. 27 Kisha baadhi ya Masadukayo wakamwendea, wale wasemao ya kwamba hakuna ufufuo, wakamwuliza, 28 wakisema, Mwalimu, Musa alituandikia ya kuwa, mtu akifiwa na ndugu yake mwenye mke, lakini hana mtoto na amtwae huyu mke, ampatie ndugu yake mzao. 29 Basi, kulikuwa na ndugu saba. Wa kwanza alioa mke, akafa hana mtoto; 30 na wa pili akamtwaa yule mke, akafa hana mtoto; 31 hata wa tatu akamwoa, na kadhalika wote saba, wakafa, wasiache watoto. 32 Mwisho akafa yule mke naye. 33 Basi, katika ufufuo atakuwa mke wa yupi? Maana aliolewa na wote saba. 34 Yesu akawaambia, Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa; 35 lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi; 36 wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo. 37 Lakini, ya kuwa wafu hufufuliwa, hata na Musa alionyesha katika sura ya Kijiti, hapo alipomtaja Bwana kuwa ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. 38 Naye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake. 39 Waandishi wengine wakajibu wakamwambia, Mwalimu, umesema vema; 40 wala hawakuthubutu kumwuliza neno baada ya hayo. 41 Akawaambia, Wasemaje watu kwamba Kristo ni Mwana wa Daudi? 42 Maana, Daudi mwenyewe asema katika chuo cha Zaburi, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, 43 Hata niwaweke adui zako Kuwa kiti cha kuwekea miguu yako. 44 Basi Daudi amwita Bwana; amekuwaje mwana wake? 45 Na watu wote walipokuwa wakimsikiliza, aliwaambia wanafunzi wake, 46 Jilindeni na waandishi, wapendao kutembea wamevaa mavazi marefu, na kusalimiwa masokoni, na kuketi mbele katika masinagogi, na viti vya mbele karamuni. 47 Wanakula nyumba za wajane, na kwa unafiki husali sala ndefu. Hao watapata hukumu iliyo kuu.

Luka 21

1 Akainua macho yake akawaona matajiri wakitia sadaka zao katika sanduku la hazina. 2 Akamwona mjane mmoja maskini akitia mle senti mbili. 3 Akasema, Hakika nawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; 4 maana, hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo. 5 Na watu kadha wa kadha walipokuwa wakiongea habari za hekalu, jinsi lilivyopambwa kwa mawe mazuri na sadaka za watu, alisema, 6 Haya mnayoyatazama, siku zitakuja ambapo halitasalia jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa. 7 Wakamwuliza wakisema, Mwalimu, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini ishara ya kuwa mambo hayo ya karibu kutukia? 8 Akasema, Angalieni, msije mkadanganyika, kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ndiye; tena, Majira yamekaribia. Basi msiwafuate hao. 9 Nanyi mtakaposikia habari za vita na fitina, msitishwe; maana, hayo hayana budi kutukia kwanza, lakini ule mwisho hauji upesi. 10 Kisha aliwaambia, Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; 11 kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi; na njaa na tauni mahali mahali; na mambo ya kutisha na ishara kuu kutoka mbinguni. 12 Lakini, kabla hayo yote hayajatokea, watawakamata na kuwaudhi; watawapeleka mbele ya masinagogi, na kuwaua magerezani, mkipelekwa mbele ya wafalme na maliwali kwa ajili ya jina langu. 13 Na hayo yatakuwa ushuhuda kwenu. 14 Basi, kusudieni mioyoni mwenu, kutofikiri-fikiri kwanza mtakavyojibu; 15 kwa sababu mimi nitawapa kinywa na hekima ambayo watesi wenu wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga. 16 Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu. 17 Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu. 18 Walakini hautapotea hata unywele mmoja wa vichwa vyenu. 19 Nanyi kwa subira yenu mtaziponya nafsi zenu. 20 Lakini, hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia. 21 Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani, na walio katikati yake wakimbilie nje, na walio katika mashamba wasiuingie. 22 Kwa kuwa siku hizo ndizo za mapatilizo, ili yatimizwe yote yaliyoandikwa. 23 Ole wao wenye mimba na wanaonyonyesha katika siku hizo! Kwa kuwa kutakuwa na shida nyingi katika nchi, na hasira juu ya taifa hili. 24 Wataanguka kwa ukali wa upanga, nao watatekwa nyara na kuchukuliwa katika mataifa yote; na Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia. 25 Tena, kutakuwa na ishara katika jua, na mwezi, na nyota; na katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa kwa uvumi wa bahari na msukosuko wake; 26 watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu. Kwa kuwa nguvu za mbinguni zitatikisika. 27 Hapo ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika wingu pamoja na nguvu na utukufu mwingi. 28 Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia. 29 Akawaambia mfano; Utazameni mtini na miti mingine yote. 30 Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. 31 Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu. 32 Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie. 33 Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe. 34 Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; 35 kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. 36 Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika haya yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu. 37 Basi, kila mchana alikuwa akifundisha hekaluni, na usiku huenda kulala katika mlima uitwao wa Mizeituni. 38 Na watu wote walikuwa wakiamka mapema waende hekaluni ili kumsikiliza.

Luka 22

1 Ikakaribia sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu, iitwayo Sikukuu ya Pasaka. 2 Na wakuu wa makuhani na waandishi walikuwa wakitafuta njia ya kumwua; maana walikuwa wakiwaogopa watu. 3 Shetani akamwingia Yuda, aitwaye Iskariote, naye ni mmoja wa wale Thenashara. 4 Akaondoka, akaenda akasema na wakuu wa makuhani na majemadari, jinsi atakavyoweza kumtia mikononi mwao. 5 Wakafurahi, wakapatana naye kumpa fedha. 6 Akakubali, akatafuta nafasi ya kumsaliti kwao pasipokuwapo mkutano. 7 Ikafika siku ya mikate isiyotiwa chachu, ambayo ilipasa kuchinja pasaka. 8 Akawatuma Petro na Yohana, akisema, Nendeni, mkatuandalie pasaka tupate kuila. 9 Wakamwambia, Wataka tuandae wapi? 10 Akawaambia, Tazama, mtakapoingia mjini mtakutana na mwanamume akichukua mtungi wa maji; mfuateni mkaingie katika nyumba atakayoingia yeye. 11 Na mtamwambia mwenye nyumba, Mwalimu akuambia, Ki wapi chumba cha wageni, nipate kula pasaka humo pamoja na wanafunzi wangu? 12 Naye atawaonyesha chumba kikubwa orofani, kimekwisha andikwa; andaeni humo. 13 Wakaenda, wakaona kama alivyowaambia, wakaiandaa pasaka. 14 Hata saa ilipofika aliketi chakulani, yeye na wale mitume pamoja naye. 15 Akawaambia, Nimetamani sana kuila pasaka hii pamoja nanyi kabla ya kuteswa kwangu; 16 kwa maana nawaambia ya kwamba siili tena hata itakapotimizwa katika ufalme wa Mungu. 17 Akapokea kikombe, akashukuru, akasema, Twaeni hiki, mgawanye ninyi kwa ninyi; 18 Maana nawaambia ya kwamba tangu sasa sinywi mazao ya mzabibu hata ufalme wa Mungu utakapokuja. 19 Akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema, Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. 20 Kikombe nacho vivyo hivyo baada ya kula; akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu. 21 Walakini, tazama, mkono wake yeye anayenisaliti upo hapa pamoja nami mezani, 22 Kwa kuwa Mwana wa Adamu aenda zake kama ilivyokusudiwa; lakini, ole wake mtu yule amsalitiye! 23 Wakaanza kuulizana wao kwa wao, ni yupi miongoni mwao atakayelitenda jambo hilo. 24 Yakatokea mashindano kati yao, kwamba ni nani anayehesabiwa kuwa mkubwa. 25 Akawaambia, Wafalme wa Mataifa huwatawala, na wenye mamlaka juu yao huitwa Wenye fadhili; 26 lakini kwenu ninyi sivyo; bali aliye mkubwa kwenu na awe kama aliye mdogo; na mwenye kuongoza kama yule atumikaye. 27 Maana aliye mkubwa ni yupi? Yeye aketiye chakulani, au yule atumikaye? Siye yule aketiye chakulani? Lakini mimi kati yenu ni kama atumikaye. 28 Nanyi ndinyi mliodumu pamoja nami katika majaribu yangu. 29 Nami nawawekea ninyi ufalme, kama vile Baba yangu alivyoniwekea mimi; 30 mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu; na kuketi katika viti vya enzi, huku mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli. 31 Akasema, Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano; 32 lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu zako. 33 Akamwambia, Bwana, niwapo pamoja nawe, mimi ni tayari kwenda gerezani au hata kifoni. 34 Akasema, Nakuambia, Petro, jogoo hatawika leo, kabla wewe hujanikana mara tatu ya kuwa hunijui. 35 Akawauliza, Je! Hapo nilipowatuma hamna mfuko, wala mkoba, wala viatu, mlipungukiwa na kitu? Wakasema, La! 36 Akawaambia, Lakini sasa mwenye mfuko na auchukue, na mkoba vivyo hivyo; naye asiye na upanga, na auze joho yake akanunue. 37 Kwa kuwa nawaambia, hayo yaliyoandikwa hayana budi kutimizwa kwangu; ya kuwa, Alihesabiwa pamoja na wahalifu. Kwa sababu yanipasayo yanao mwisho wake. 38 Wakasema, Bwana, tazama, hapa pana panga mbili. Akawaambia, Basi. 39 Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. 40 Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. 41 Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, 42 akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. 43 Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu. 44 Naye kwa vile alivyokuwa katika dhiki, akazidi sana kuomba; hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchini. 45 Alipoondoka katika kuomba kwake, akawajia wanafunzi wake, akawakuta wamelala usingizi kwa huzuni. 46 Akawaambia, Mbona mmelala usingizi? Ondokeni, mkaombe, msije mkaingia majaribuni. 47 Basi alipokuwa katika kusema, tazama, mkutano wa watu, na yule aitwaye Yuda, ambaye ni mmoja wa wale Thenashara, amewatangulia. Akamkaribia Yesu ili kumbusu. 48 Yesu akamwambia, Yuda, wamsaliti Mwana wa Adamu kwa kumbusu? 49 Na wale waliokuwa karibu naye walipoona yatakayotukia, walisema, Bwana, tuwapige kwa upanga? 50 Mmoja wao akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio la kuume. 51 Yesu akajibu akasema, Mwe radhi kwa hili. Akamgusa sikio, akamponya. 52 Yesu akawaambia wakuu wa makuhani, na maakida wa hekalu, na wazee, waliokuja juu yake, Je! Mmekuja wenye panga na marungu kama kukamata mnyang'anyi? 53 Kila siku nilipokuwa pamoja nanyi hekaluni hamkuninyoshea mikono, lakini hii ndiyo saa yenu, na mamlaka ya giza. 54 Wakamkamata, wakamchukua, wakaenda naye nyumbani kwa Kuhani Mkuu. Na Petro alimfuata kwa mbali. 55 Na walipokwisha washa moto katikati ya kiwanja, waliketi pamoja, naye Petro akaketi kati yao. 56 Ndipo mjakazi mmoja akamwona ameketi mwangani, akamkazia macho akasema, Na huyu alikuwa pamoja naye. 57 Akakana, akisema, Ee mwanamke, simjui. 58 Baadaye kitambo mtu mwingine alimwona akasema, Wewe nawe u mmoja wao. Petro akasema, Ee mtu, si mimi. 59 Halafu, yapata saa moja, mtu mwingine alikaza kusema, Hakika na huyu alikuwa pamoja naye, kwa kuwa yeye pia ni Mgalilaya. 60 Petro akasema, Ee mtu, sijui usemalo. Na papo hapo alipokuwa katika kusema, jogoo aliwika. 61 Bwana akageuka akamtazama Petro. Petro akalikumbuka lile neno la Bwana jinsi alivyomwambia, Leo kabla hajawika jogoo utanikana mara tatu. 62 Akatoka nje akalia kwa majonzi. 63 Na wale watu waliokuwa wakimshika Yesu walimfanyia dhihaka, wakampiga. 64 Wakamfunika macho, kisha wakamwuliza-uliza wakisema, Tabiri, ni nani aliyekupiga? 65 Wakamtolea na maneno mengine mengi ya kumtukana. 66 Hata kulipokucha, walikutanika jamii ya wazee, na wakuu wa makuhani, na waandishi, wakamleta katika baraza yao, wakisema, 67 Kama wewe ndiwe Kristo, tuambie. Akawaambia, Nijapowaambia, hamtasadiki kabisa. 68 Tena, nikiwauliza, hamtajibu. 69 Lakini tangu sasa Mwana wa Adamu atakuwa ameketi upande wa kuume wa Mungu Mwenyezi. 70 Wakasema wote, Basi, wewe ndiwe Mwana wa Mungu? Akawaambia, Ninyi mwasema kwamba mimi ndiye. 71 Wakasema, Basi, tuna haja gani tena ya ushuhuda? Maana, sisi wenyewe tumesikia maneno ya kinywa chake.

Luka 23

1 Wakasimama mkutano wote, wakampeleka kwa Pilato. 2 Wakaanza kumshitaki, wakisema, Tumemwona huyu akipotosha taifa letu, na kuwazuia watu wasimpe Kaisari kodi, akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo, mfalme. 3 Pilato akamwuliza, akisema, Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi? Akajibu akamwambia, Wewe wasema. 4 Pilato akawaambia wakuu wa makuhani na makutano, Sioni neno lililo ovu katika mtu huyu. 5 Nao walikaza sana, wakisema, Huwataharakisha watu, akifundisha katika Uyahudi yote, tokea Galilaya mpaka huku. 6 Pilato aliposikia hayo aliuliza kama huyu ni mtu wa Galilaya. 7 Na alipopata habari ya kuwa yu chini ya mamlaka ya Herode, alimpeleka kwa Herode, kwa kuwa yeye naye alikuwapo Yerusalemu siku zile. 8 Na Herode alipomwona Yesu alifurahi sana, kwa sababu alikuwa akitaka sana kumwona tangu siku nyingi, maana amesikia habari zake, akataraji kuona ishara iliyofanywa na yeye. 9 Akamwuliza maneno mengi, yeye asimjibu lo lote. 10 Wakuu wa makuhani na waandishi wakasimama wakamshitaki kwa nguvu sana. 11 Basi Herode akamfanya duni, pamoja na askari zake, akamdhihaki, na kumvika mavazi mazuri; kisha akamrudisha kwa Pilato. 12 Basi siku ile ile Herode na Pilato walipatana kwa urafiki kwa maana hapo kwanza walikuwa na uadui wao kwa wao. 13 Na Pilato akawakutanisha wakuu wa makuhani, na wakubwa, na watu, 14 akawaambia, Mtu huyu mmemleta kwangu kana kwamba anapotosha watu; nami, tazama, nimeamua mambo yake mbele yenu, ila sikuona kwake kosa lo lote katika mambo hayo mliyomshitaki; 15 wala hata Herode, kwa maana amemrudisha kwetu; basi tazama, hakuna neno lo lote alilolitenda lipasalo kufa. 16 Kwa hiyo nitamrudi, kisha nitamfungua. 17 Maana ilimlazimu kuwafungulia mfungwa mmoja wakati wa sikukuu. 18 Wakapiga kelele wote pamoja, wakisema, Mwondoe huyu, utufungulie Baraba. 19 Naye ni mtu aliyetupwa gerezani kwa ajili ya fitina iliyotokea mjini, na kwa uuaji 20 Basi Pilato alisema nao mara ya pili, kwa vile alivyotaka kumfungua Yesu. 21 Lakini wakapiga kelele, wakisema, Msulibishe. Msulibishe. 22 Akawaambia mara ya tatu, Kwa sababu gani? Huyu ametenda uovu gani? Sikuona kwake hata neno lipasalo kufa. Basi nikiisha kumrudi nitamfungua. 23 Lakini wakatoa sauti zao kwa nguvu sana, wakitaka asulibiwe. Sauti zao zikashinda. 24 Pilato akahukumu kwamba haja yao ifanyike. 25 Akamfungua yule aliyetupwa gerezani kwa ajili ya fitina na uuaji, yule waliyemtaka, akamtoa Yesu wamfanyie watakavyo. 26 Na walipokuwa wakimwondoa walimkamata mtu mmoja, Simoni Mkirene, aliyekuwa ametoka shamba, wakamtwika msalaba, auchukue nyuma yake Yesu. 27 Mkutano mkubwa wa watu wakamfuata, na wanawake waliokuwa wakijipiga vifua na kumwombolezea. 28 Yesu akawageukia, akasema, Enyi binti za Yerusalemu, msinililie mimi, bali jililieni nafsi zenu na watoto wenu. 29 Kwa maana tazama, siku zitakuja watakaposema, Heri walio tasa, na matumbo yasiyozaa, na maziwa yasiyonyonyesha. 30 Ndipo watakapoanza kuiambia milima, Tuangukieni, na vilima, Tufunikeni. 31 Kwa kuwa kama wakitenda mambo haya katika mti mbichi, itakuwaje katika mkavu? 32 Wakapelekwa na wawili wengine, wahalifu, wauawe pamoja naye. 33 Na walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, ndipo walipomsulibisha yeye, na wale wahalifu, mmoja upande wa kuume, na mmoja upande wa kushoto. 34 Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa mavazi yake, wakipiga kura. 35 Watu wakasimama wakitazama. Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. 36 Wale askari nao wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki, 37 huku wakisema, Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe. 38 Na juu yake palikuwa na anwani; HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI. 39 Na mmoja wa wale wahalifu waliotungikwa alimtukana, akisema, Je! Wewe si Kristo? Jiokoe nafsi yako na sisi. 40 Lakini yule wa pili akamjibu akamkemea, akisema, Wewe humwogopi hata Mungu, nawe u katika hukumu iyo hiyo? 41 Nayo ni haki kwetu sisi, kwa kuwa tunapokea malipo tuliyostahili kwa matendo yetu; bali huyu hakutenda lo lote lisilofaa. 42 Kisha akasema, Ee Yesu, nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako. 43 Yesu akamwambia, Amin, nakuambia, leo hivi utakuwa pamoja nami peponi. 44 Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, 45 jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. 46 Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu. 47 Alipokwisha kusema hayo alikata roho. Yule akida alipoona yaliyotukia, alimtukuza Mungu, akisema, Hakika yake, mtu huyu alikuwa mwenye haki. 48 Na makutano yote ya watu waliokuwa wamekutanika kutazama mambo hayo, walipoona yaliyotendeka, wakaenda zao kwao, wakijipiga-piga vifua. 49 Na wote waliojuana naye, na wale wanawake walioandamana naye toka Galilaya, wakasimama kwa mbali, wakitazama mambo hayo. 50 Na tazama, akatoka mtu mmoja, jina lake Yusufu, ambaye ni mtu wa baraza, mtu mwema, mwenye haki; 51 (wala hakulikubali shauri na tendo lao), naye ni mtu wa Arimathaya, mji mmoja wa Wayahudi, tena anautazamia ufalme wa Mungu; 52 mtu huyo alikwenda kwa Pilato, akataka kupewa mwili wa Yesu. 53 Akaushusha, akauzinga sanda ya kitani, akauweka katika kaburi lililochongwa mwambani, ambalo hajalazwa mtu bado ndani yake. 54 Na siku ile ilikuwa siku ya Maandalio, na sabato ikaanza kuingia. 55 Na wale wanawake waliokuja naye toka Galilaya walifuata, wakaliona kaburi, na jinsi mwili wake ulivyowekwa. 56 Wakarudi, wakafanya tayari manukato na marhamu. Na siku ya sabato walistarehe kama ilivyoamriwa.

Luka 24

1 Hata siku ya kwanza ya juma, ilipoanza kupambazuka, walikwenda kaburini, wakiyaleta manukato waliyoweka tayari. 2 Wakalikuta lile jiwe limevingirishwa mbali na kaburi, 3 Wakaingia, wasiuone mwili wa Bwana Yesu. 4 Ikawa walipokuwa wakifadhaika kwa ajili ya neno hilo, tazama, watu wawili walisimama karibu nao, wamevaa nguo za kumeta-meta; 5 nao walipoingiwa na hofu na kuinama kifudifudi hata nchi, hao waliwaambia, Kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu? 6 Hayupo hapa, amefufuka. Kumbukeni alivyosema nanyi alipokuwa akaliko Galilaya, 7 akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kutiwa mikononi mwa wenye dhambi, na kusulibiwa, na kufufuka siku ya tatu. 8 Wakayakumbuka maneno yake. 9 Wakaondoka kaburini, wakarudi; wakawaarifu wale kumi na mmoja na wengine wote habari za mambo hayo yote. 10 Nao ni Mariamu Magdalene, na Yoana, na Mariamu mamaye Yakobo, na wale wanawake wengine waliokuwa pamoja nao; 11 hao waliwaambia mitume habari ya mambo hayo. 12 Maneno yao yakaonekana kuwa kama upuzi kwao, wala hawakuwasadiki. Lakini Petro aliondoka akaenda mbio hata kaburini, akainama akachungulia ndani, akaviona vile vitambaa vya sanda tu; akaenda zake akiyastaajabia yaliyotukia. 13 Na tazama, siku ile ile watu wawili miongoni mwao walikuwa wakienda kijiji kimoja, jina lake Emau, kilichokuwa mbali na Yerusalemu kama mwendo wa saa mbili. 14 Nao walikuwa wakizungumza wao kwa wao habari za mambo hayo yote yaliyotukia. 15 Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao. 16 Macho yao yakafumbwa wasimtambue. 17 Akawaambia, Ni maneno gani haya mnayosemezana hivi mnapotembea? Wakasimama wamekunja nyuso zao. 18 Akajibu mmoja wao, jina lake Kleopa, akamwambia, Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi? 19 Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; 20 tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. 21 Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli. Zaidi ya hayo yote, leo ni siku ya tatu tangu yalipotendeka mambo hayo; 22 tena, wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha, waliokwenda kaburini asubuhi na mapema, 23 wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba yu hai. 24 Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona. 25 Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! 26 Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? 27 Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe. 28 Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya kama anataka kuendelea mbele. 29 Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. 30 Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. 31 Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao. 32 Wakaambiana, Je! Mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko? 33 Wakaondoka saa ile ile, wakarejea Yerusalemu, wakawakuta wale kumi na mmoja wamekutanika, wao na wale waliokuwa pamoja nao, 34 wakisema, Bwana amefufuka kweli kweli, naye amemtokea Simoni. 35 Nao waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate. 36 Na walipokuwa katika kusema habari hiyo, yeye mwenyewe alisimama katikati yao, akawaambia, Amani iwe kwenu. 37 Wakashituka, wakaogopa sana, wakidhani ya kwamba wanaona roho. 38 Akawaambia, Mbona mnafadhaika? Na kwa nini mnaona shaka mioyoni mwenu? 39 Tazameni mikono yangu na miguu yangu, ya kuwa ni mimi mwenyewe. Nishikenishikeni, mwone; kwa kuwa roho haina mwili na mifupa kama mnavyoniona mimi kuwa nayo. 40 Na baada ya kusema hayo aliwaonyesha mikono yake na miguu yake. 41 Basi walipokuwa hawajaamini kwa furaha, huku wakistaajabu, aliwaambia, Mna chakula cho chote hapa? 42 Wakampa kipande cha samaki wa kuokwa. 43 Akakitwaa, akala mbele yao. 44 Kisha akawaambia, Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii na Zaburi. 45 Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko. 46 Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; 47 na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. 48 Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. 49 Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu. 50 Akawaongoza mpaka Bethania, akainua mikono yake akawabariki. 51 Ikawa katika kuwabariki, alijitenga nao; akachukuliwa juu mbinguni. 52 Wakamwabudu; kisha wakarudi Yerusalemu wenye furaha kuu. 53 Nao walikuwa daima ndani ya hekalu, wakimsifu Mungu.

Yohana 1

1 Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. 2 Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. 3 Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. 4 Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu. 5 Nayo nuru yang'aa gizani, wala giza halikuiweza. 6 Palitokea mtu, ametumwa kutoka kwa Mungu, jina lake Yohana. 7 Huyo alikuja kwa ushuhuda, ili aishuhudie ile nuru, wote wapate kuamini kwa yeye. 8 Huyo hakuwa ile nuru, bali alikuja ili aishuhudie ile nuru. 9 Kulikuwako Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu, akija katika ulimwengu. 10 Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. 11 Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea. 12 Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; 13 waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu. 14 Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli. 15 Yohana alimshuhudia, akapaza sauti yake akasema, Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Ajaye nyuma yangu amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu. 16 Kwa kuwa katika utimilifu wake sisi sote tulipokea, na neema juu ya neema. 17 Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo. 18 Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote; Mungu Mwana pekee aliye katika kifua cha Baba, huyu ndiye aliyemfunua. 19 Na huu ndio ushuhuda wake Yohana, Wayahudi walipotuma kwake makuhani na Walawi kutoka Yerusalemu ili wamwulize, Wewe u nani? 20 Naye alikiri, wala hakukana; alikiri kwamba, Mimi siye Kristo. 21 Wakamwuliza, Ni nini basi? U Eliya wewe? Akasema, Mimi siye. Wewe u nabii yule? Akajibu, La. 22 Basi wakamwambia, U nani? Tuwape majibu wale waliotupeleka. Wanenaje juu ya nafsi yako? 23 Akasema, Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, Inyosheni njia ya Bwana! Kama vile alivyonena nabii Isaya. 24 Nao wale waliotumwa walikuwa wametoka kwa Mafarisayo. 25 Wakamwuliza, wakamwambia, Mbona basi wabatiza, ikiwa wewe si Kristo, wala Eliya, wala nabii yule? 26 Yohana akawajibu akisema, Mimi nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi. 27 Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake. 28 Hayo yalifanyika huko Bethania ng'ambo ya Yordani, alikokuwako Yohana akibatiza. 29 Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu! 30 Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu. 31 Wala mimi sikumjua; lakini kusudi adhihirishwe kwa Israeli ndiyo maana mimi nalikuja nikibatiza kwa maji. 32 Tena Yohana akashuhudia akisema, Nimemwona Roho akishuka kama hua kutoka mbinguni; naye akakaa juu yake. 33 Wala mimi sikumjua; lakini yeye aliyenipeleka kubatiza kwa maji, huyo aliniambia, Yeye ambaye utamwona Roho akishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye abatizaye kwa Roho Mtakatifu. 34 Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu. 35 Tena siku ya pili yake Yohana alikuwa amesimama pamoja na wawili katika wanafunzi wake. 36 Akamtazama Yesu akitembea, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu! 37 Wale wanafunzi wawili wakamsikia akinena, wakamfuata Yesu. 38 Yesu aligeuka, akawaona wakimfuata, akawaambia, Mnatafuta nini? Wakamwambia, Rabi, (maana yake, Mwalimu), unakaa wapi? 39 Akawaambia, Njoni, nanyi mtaona. Wakaenda, wakaona akaapo, wakakaa kwake siku ile. Nayo ilikuwa yapata saa kumi. 40 Andrea, nduguye Simoni Petro, alikuwa mmoja wa wale wawili waliomsikia Yohana na kumfuata Yesu. 41 Huyo akamwona kwanza Simoni, ndugu yake mwenyewe, akamwambia, Tumemwona Masihi (maana yake, Kristo). 42 Akampeleka kwa Yesu. Naye Yesu akamtazama, akasema, Wewe u Simoni, mwana wa Yohana; nawe utaitwa Kefa (tafsiri yake Petro, au Jiwe). 43 Siku ya pili yake alitaka kuondoka kwenda Galilaya, naye akamwona Filipo. Yesu akamwambia, Nifuate. 44 Naye Filipo alikuwa mtu wa Bethsaida, mwenyeji wa mji wa Andrea na Petro. 45 Filipo akamwona Nathanaeli, akamwambia, Tumemwona yeye aliyeandikiwa na Musa katika torati, na manabii, Yesu, mwana wa Yusufu, mtu wa Nazareti. 46 Nathanaeli akamwambia, Laweza neno jema kutoka Nazareti? Filipo akamwambia, Njoo uone. 47 Basi Yesu akamwona Nathanaeli anakuja kwake, akanena habari zake, Tazama, Mwisraeli kweli kweli, hamna hila ndani yake. 48 Nathanaeli akamwambia, Umepataje kunitambua? Yesu akajibu, akamwambia, Kabla Filipo hajakuita, ulipokuwapo chini ya mtini nilikuona. 49 Nathanaeli akamjibu, Rabi, wewe u Mwana wa Mungu, ndiwe Mfalme wa Israeli. 50 Yesu akajibu, akamwambia, Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya. 51 Akamwambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu.

Yohana 2

1 Na siku ya tatu palikuwa na arusi huko Kana, mji wa Galilaya; naye mama yake Yesu alikuwapo. 2 Yesu naye alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake. 3 Hata divai ilipowatindikia, mamaye Yesu akamwambia, Hawana divai. 4 Yesu akamwambia, Mama, tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia. 5 Mamaye akawaambia watumishi, Lo lote atakalowaambia, fanyeni. 6 Basi kulikuwako huko mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha, kila moja lapata kadiri ya nzio mbili tatu. 7 Yesu akawaambia, Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata juu. 8 Akawaambia, Sasa tekeni, mkampelekee mkuu wa meza. Wakapeleka. 9 Naye mkuu wa meza alipoyaonja yale maji yaliyopata kuwa divai, (wala asijue ilikotoka, lakini watumishi walijua, wale walioyateka yale maji), yule mkuu wa meza alimwita bwana arusi, 10 akamwambia, Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa. 11 Mwanzo huo wa ishara Yesu aliufanya huko Kana ya Galilaya, akaudhihirisha utukufu wake, nao wanafunzi wake wakamwamini. 12 Baada ya hayo akashuka mpaka Kapernaumu, yeye na mama yake na ndugu zake na wanafunzi wake; wakakaa huko siku si nyingi. 13 Na Pasaka ya Wayahudi ilikuwa karibu; naye Yesu akakwea mpaka Yerusalemu. 14 Akaona pale hekaluni watu waliokuwa wakiuza ng'ombe na kondoo na njiwa, na wenye kuvunja fedha wameketi. 15 Akafanya kikoto cha kambaa, akawatoa wote katika hekalu, na kondoo na ng'ombe; akamwaga fedha za wenye kuvunja fedha, akazipindua meza zao; 16 akawaambia wale waliokuwa wakiuza njiwa, Yaondoeni haya; msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara. 17 Wanafunzi wake wakakumbuka ya kuwa imeandikwa, Wivu wa nyumba yako utanila. 18 Basi Wayahudi wakajibu, wakamwambia, Ni ishara gani utuonyeshayo, kwamba unafanya haya? 19 Yesu akajibu, akawaambia, Livunjeni hekalu hili, nami katika siku tatu nitalisimamisha. 20 Basi Wayahudi wakasema, Hekalu hili lilijengwa katika muda wa miaka arobaini na sita, nawe utalisimamisha katika siku tatu? 21 Lakini yeye alinena habari za hekalu la mwili wake. 22 Basi alipofufuka katika wafu, wanafunzi wake wakakumbuka ya kuwa alisema hivi, wakaliamini lile andiko na lile neno alilolinena Yesu. 23 Hata alipokuwapo Yerusalemu kwenye sikukuu wakati wa Pasaka, watu wengi waliamini jina lake, walipoziona ishara zake alizozifanya. 24 Lakini Yesu hakujiaminisha kwao; kwa kuwa yeye aliwajua wote; 25 na kwa sababu hakuwa na haja ya mtu kushuhudia habari za mwanadamu; kwa maana yeye mwenyewe alijua yaliyomo ndani ya mwanadamu.

Yohana 3

1 Basi palikuwa na mtu mmoja wa Mafarisayo, jina lake Nikodemo, mkuu wa Wayahudi. 2 Huyo alimjia usiku, akamwambia, Rabi, twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa Mungu yu pamoja naye. 3 Yesu akajibu, akamwambia, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu. 4 Nikodemo akamwambia, Awezaje mtu kuzaliwa, akiwa mzee? Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa? 5 Yesu akajibu, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu. 6 Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho. 7 Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, Hamna budi kuzaliwa mara ya pili. 8 Upepo huvuma upendako, na sauti yake waisikia, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda; kadhalika na hali yake kila mtu aliyezaliwa kwa Roho. 9 Nikodemo akajibu, akamwambia, Yawezaje kuwa mambo haya? 10 Yesu akajibu, akamwambia, Je! Wewe u mwalimu wa Israeli, na mambo haya huyafahamu? 11 Amin, amin, nakuambia kwamba, Lile tulijualo twalinena, na lile tuliloliona twalishuhudia; wala ushuhuda wetu hamwukubali. 12 Ikiwa nimewaambia mambo ya duniani, wala hamsadiki, mtasadiki wapi niwaambiapo mambo ya mbinguni? 13 Wala hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu. 14 Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; 15 ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye. 16 Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. 17 Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. 18 Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu. 19 Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. 20 Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. 21 Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu. 22 Baada ya hayo Yesu na wanafunzi wake walikwenda mpaka nchi ya Uyahudi; akashinda huko pamoja nao, akabatiza. 23 Yohana naye alikuwa akibatiza huko Ainoni, karibu na Salimu, kwa sababu huko kulikuwa na maji tele; na watu wakamwendea, wakabatizwa. 24 Maana Yohana alikuwa hajatiwa gerezani. 25 Basi palitokea mashindano ya wanafunzi wa Yohana na Myahudi mmoja juu ya utakaso. 26 Wakamwendea Yohana, wakamwambia, Rabi, yeye aliyekuwa pamoja nawe ng'ambo ya Yordani, yeye uliyemshuhudia, tazama, huyo anabatiza na watu wote wanamwendea. 27 Yohana akajibu, akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni. 28 Ninyi wenyewe mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake. 29 Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi. 30 Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua. 31 Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote. 32 Yale aliyoyaona na kuyasikia ndiyo anayoyashuhudia, wala hakuna anayeukubali ushuhuda wake. 33 Yeye aliyeukubali ushuhuda wake ametia muhuri ya kwamba Mungu ni kweli. 34 Kwa kuwa yeye aliyetumwa na Mungu huyanena maneno ya Mungu; kwa sababu hamtoi Roho kwa kipimo. 35 Baba ampenda Mwana, naye amempa vyote mkononi mwake. 36 Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.

Yohana 4

1 Kwa hiyo Bwana, alipofahamu ya kuwa Mafarisayo wamesikia ya kwamba, Yesu anafanya wanafunzi wengi kuliko Yohana, na kuwabatiza, 2 (lakini Yesu mwenyewe hakubatiza, bali wanafunzi wake,) 3 aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya. 4 Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria. 5 Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe. 6 Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. 7 Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. 8 Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. 9 Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) 10 Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. 11 Yule mwanamke akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? 12 Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake? 13 Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; 14 walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele. 15 Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. 16 Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. 17 Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; 18 kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. 19 Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! 20 Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. 21 Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. 22 Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi. 23 Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. 24 Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. 25 Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. 26 Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye. 27 Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? 28 Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, 29 Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? 30 Basi wakatoka mjini, wakamwendea. 31 Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. 32 Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. 33 Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula? 34 Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. 35 Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. 36 Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. 37 Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. 38 Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao. 39 Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. 40 Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. 41 Watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. 42 Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu. 43 Na baada ya siku mbili hizo akaondoka huko, akaenda Galilaya. 44 Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hapati heshima katika nchi yake mwenyewe. 45 Basi alipotoka Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu. 46 Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. 47 Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. 48 Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa? 49 Yule diwani akamwambia, Bwana, ushuke asijakufa mtoto wangu. 50 Yesu akamwambia, Enenda; mwanao yu hai. Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia. 51 Hata alipokuwa akishuka, watumwa wake walimlaki, wakisema ya kwamba mtoto wake yu hai. 52 Basi akawauliza habari ya saa alipoanza kuwa hajambo; nao wakamwambia, Jana, saa saba, homa ilimwacha. 53 Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile aliyoambiwa na Yesu, Mwanao yu hai. Akaamini yeye na wote wa nyumbani mwake. 54 Hiyo ni ishara ya pili aliyoifanya Yesu, alipokuwa ametoka Uyahudi kufika Galilaya.

Yohana 5

1 Baada ya hayo palikuwa na sikukuu ya Wayahudi; naye Yesu akakwea kwenda Yerusalemu. 2 Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao matano. 3 Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza, wakingoja maji yachemke. 4 Kwa maana kuna wakati ambapo malaika hushuka, akaingia katika ile birika, akayatibua maji. Basi yeye aliyeingia wa kwanza baada ya maji kutibuliwa, akapona ugonjwa wote uliokuwa umempata. 5 Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. 6 Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? 7 Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu. 8 Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende. 9 Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda. Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo. 10 Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwambia yule aliyeponywa, Leo ni sabato, wala si halali kwako kujitwika godoro. 11 Akawajibu, Yeye aliyenifanya kuwa mzima ndiye aliyeniambia, Jitwike godoro lako, uende. 12 Basi wakamwuliza, Yule aliyekuambia, Jitwike, uende, ni nani? 13 Lakini yule mtu aliyeponywa hakumjua ni nani; maana Yesu alikuwa amejitenga, kwa sababu palikuwa na watu wengi mahali pale. 14 Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, Angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi. 15 Yule mtu akaenda zake, akawapasha habari Wayahudi ya kwamba ni Yesu aliyemfanya kuwa mzima. 16 Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwudhi Yesu, kwa kuwa alitenda hayo siku ya sabato. 17 Akawajibu, Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi. 18 Basi kwa sababu hiyo Wayahudi walizidi kutaka kumwua, kwa kuwa hakuivunja sabato tu, bali pamoja na hayo alimwita Mungu Baba yake, akijifanya sawa na Mungu. Basi Yesu akajibu, akawaambia, Amin, amin, nawaambia, 19 Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile. 20 Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizo atamwonyesha, ili ninyi mpate kustaajabu. 21 Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana awahuisha wale awatakao. 22 Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote; 23 ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka. 24 Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani. 25 Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai. 26 Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. 27 Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. 28 Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. 29 Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu. 30 Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka. 31 Mimi nikijishuhudia mwenyewe, ushuhuda wangu si kweli. 32 Yuko mwingine anayenishuhudia; nami najua ya kuwa ushuhuda wake anaonishuhudia ni kweli. 33 Ninyi mlituma watu kwa Yohana, naye akaishuhudia kweli. 34 Lakini mimi siupokei ushuhuda kwa wanadamu; walakini ninasema haya ili ninyi mpate kuokoka. 35 Yeye alikuwa taa iwakayo na kung'aa, nanyi mlipenda kuishangilia nuru yake kwa muda. 36 Lakini ushuhuda nilio nao mimi ni mkubwa kuliko ule wa Yohana; kwa kuwa zile kazi alizonipa Baba ili nizimalize, kazi hizo zenyewe ninazozitenda, zanishuhudia ya kwamba Baba amenituma. 37 Naye Baba aliyenipeleka amenishuhudia. Sauti yake hamkuisikia wakati wo wote, wala sura yake hamkuiona. 38 Wala neno lake hamnalo likikaa ndani yenu, kwa kuwa ninyi hammwamini yule aliyetumwa na yeye. 39 Mwayachunguza maandiko, kwa sababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; na hayo ndiyo yanayonishuhudia. 40 Wala hamtaki kuja kwangu mpate kuwa na uzima. 41 Mimi siupokei utukufu kwa wanadamu. 42 Walakini nimewajua ninyi ya kuwa hamna upendo wa Mungu ndani yenu. 43 Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu, wala ninyi hamnipokei; mwingine akija kwa jina lake mwenyewe, mtampokea huyo. 44 Mwawezaje kuamini ninyi mnaopokeana utukufu ninyi kwa ninyi, na utukufu ule utokao kwa Mungu aliye wa pekee hamwutafuti? 45 Msidhani kwamba mimi nitawashitaki kwa Baba; yuko anayewashitaki, ndiye Musa, mnayemtumaini ninyi. 46 Kwa maana kama mngalimwamini Musa, mngeniamini mimi; kwa sababu yeye aliandika habari zangu. 47 Lakini msipoyaamini maandiko yake, mtayaamini wapi maneno yangu?

Yohana 6

1 Baada ya hayo Yesu alikwenda zake ng'ambo ya Bahari ya Galilaya, nayo ndiyo ya Tiberia. 2 Na mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa. 3 Naye Yesu akakwea mlimani, akaketi huko pamoja na wanafunzi wake. 4 Na Pasaka, sikukuu ya Wayahudi, ilikuwa karibu. 5 Basi Yesu alipoinua macho yake akaona mkutano mkuu wanakuja kwake, alimwambia Filipo, Tununue wapi mikate, ili hawa wapate kula? 6 Na hilo alilinena ili kumjaribu; kwa maana alijua mwenyewe atakalotenda. 7 Filipo akamjibu, Mikate ya dinari mia mbili haiwatoshi, kila mmoja apate kidogo tu. 8 Wanafunzi wake mmojawapo, Andrea, nduguye Simoni Petro, akamwambia, 9 Yupo hapa mtoto, yuna mikate mitano ya shayiri na samaki wawili, lakini hivi ni nini kwa watu wengi kama hawa? 10 Yesu akasema, Waketisheni watu. Na mahali pale palikuwa na majani tele. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu tano jumla yao. 11 Basi Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru, akawagawia walioketi; na kadhalika katika wale samaki kwa kadiri walivyotaka. 12 Nao waliposhiba, aliwaambia wanafunzi wake, Kusanyeni vipande vilivyobaki, kisipotee cho chote. 13 Basi wakavikusanya, wakajaza vikapu kumi na viwili, vipande vya mikate mitano ya shayiri vilivyowabakia wale waliokula. 14 Basi watu wale, walipoiona ishara aliyoifanya, walisema, Hakika huyu ni nabii yule ajaye ulimwenguni. 15 Kisha Yesu, hali akitambua ya kuwa walitaka kuja kumshika ili wamfanye mfalme, akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake. 16 Hata ilipokuwa jioni wanafunzi wake wakatelemka baharini 17 wakapanda chomboni, wakaanza kuivuka bahari kwenda Kapernaumu. Nako kumekwisha kuwa giza, wala Yesu hajawafikia. 18 Na bahari ikaanza kuchafuka kwa kuvuma upepo mkuu. 19 Basi wakavuta makasia kadiri ya maili tatu nne, wakamwona Yesu anakwenda juu ya bahari na kukikaribia chombo; wakaogopa. 20 Naye akawaambia, Ni mimi, msiogope. 21 Basi wakataka kumpokea chomboni; na mara hiyo chombo kikaifikilia nchi waliyokuwa wakiiendea. 22 Siku ya pili yake mkutano waliosimama ng'ambo ya bahari waliona ya kuwa hakuna mashua nyingine huko ila moja, tena ya kuwa Yesu hakuingia katika mashua ile pamoja na wanafunzi wake, bali wanafunzi wake walikwenda peke yao. 23 (Walakini zikaja mashua nyingine kutoka Tiberia mpaka karibu na mahali pale walipokula mikate, wakati Bwana aliposhukuru.) 24 Basi mkutano, walipoona ya kuwa Yesu hayuko huko wala wanafunzi wake, waliingia mashuani wenyewe, wakaenda Kapernaumu wakimtafuta Yesu. 25 Hata walipomwona ng'ambo ya bahari, walimwambia, Rabi, wewe umekuja lini hapa? 26 Yesu akawajibu, akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba. 27 Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu. 28 Basi wakamwambia, Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu? 29 Yesu akajibu, akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye. 30 Wakamwambia, Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani? 31 Baba zetu waliila mana jangwani kama vile ilivyoandikwa, Aliwapa chakula cha mbinguni ili wale. 32 Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni. 33 Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima. 34 Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki. 35 Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe. 36 Lakini naliwaambia ya kwamba mmeniona wala hamwamini. 37 Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe. 38 Kwa kuwa mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka. 39 Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, ya kwamba katika wote alionipa nisimpoteze hata mmoja, bali nimfufue siku ya mwisho. 40 Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. 41 Basi Wayahudi wakamnung'unikia, kwa sababu alisema, Mimi ni chakula kilichoshuka kutoka mbinguni. 42 Wakasema, Je! Huyu siye Yesu, mwana wa Yusufu, ambaye twamjua babaye na mamaye? Sasa asemaje huyu, Nimeshuka kutoka mbinguni? 43 Basi Yesu akajibu, akawaambia, Msinung'unike ninyi kwa ninyi. 44 Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. 45 Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu. 46 Si kwamba mtu amemwona Baba, ila yeye atokaye kwa Mungu; huyo ndiye aliyemwona Baba. 47 Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele. 48 Mimi ndimi chakula cha uzima. 49 Baba zenu waliila mana jangwani; wakafa. 50 Hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni, kwamba mtu akile wala asife. 51 Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu. 52 Basi Wayahudi walishindana wao kwa wao wakisema, Awezaje mtu huyu kutupa sisi mwili wake ili tuule? 53 Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. 54 Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. 55 Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. 56 Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. 57 Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi. 58 Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa walivyokula, wakafa; bali akilaye chakula hicho ataishi milele. 59 Maneno hayo aliyasema katika sinagogi, alipokuwa akifundisha, huko Kapernaumu. 60 Basi watu wengi miongoni mwa wanafunzi wake waliposikia, walisema, Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia? 61 Naye Yesu akafahamu nafsini mwake ya kuwa wanafunzi wake wanalinung'unikia neno hilo, akawaambia, Je! Neno hili linawakwaza? 62 Itakuwaje basi, mmwonapo Mwana wa Adamu akipaa huko alikokuwako kwanza? 63 Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima. 64 Lakini kuna wengine miongoni mwenu wasioamini. Kwa maana Yesu alijua tangu mwanzo ni nani wasioamini, naye ni nani atakayemsaliti. 65 Akasema, Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu. 66 Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena. 67 Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? 68 Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. 69 Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu. 70 Yesu akawajibu, Je! Mimi sikuwachagua ninyi Thenashara, na mmoja wenu ni shetani? 71 Alimnena Yuda, mwana wa Simoni Iskariote; maana huyo ndiye atakayemsaliti; naye ni mmojawapo wa wale Thenashara.

Yohana 7

1 Na baada ya hayo Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuwa wakitafuta kumwua. 2 Na sikukuu ya Wayahudi, Sikukuu ya Vibanda, ilikuwa karibu. 3 Basi ndugu zake wakamwambia, Ondoka hapa, uende Uyahudi, wanafunzi wako nao wapate kuzitazama kazi zako unazozifanya. 4 Kwa maana hakuna mtu afanyaye neno kwa siri, naye mwenyewe ataka kujulikana. Ukifanya mambo haya, basi jidhihirishe kwa ulimwengu. 5 Maana hata nduguze hawakumwamini. 6 Basi Yesu akawaambia, Haujafika bado wakati wangu; ila wakati wenu sikuzote upo. 7 Ulimwengu hauwezi kuwachukia ninyi; bali hunichukia mimi, kwa sababu mimi naushuhudia ya kuwa kazi zake ni mbovu. 8 Kweeni ninyi kwenda kula sikukuu; mimi sikwei bado kwenda kula sikukuu hii, kwa kuwa haujatimia wakati wangu. 9 Naye alipokwisha kuwaambia hayo, alikaa vivi hivi huko Galilaya. 10 Hata ndugu zake walipokwisha kukwea kuiendea sikukuu, ndipo yeye naye alipokwea, si kwa wazi bali kana kwamba kwa siri. 11 Basi Wayahudi wakamtafuta kwenye sikukuu, wakasema, Yuko wapi yule? 12 Kukawa na manung'uniko mengi katika makutano juu yake. Wengine wakasema, Ni mtu mwema. Na wengine wakasema, Sivyo; bali anawadanganya makutano. 13 Walakini hakuna mtu aliyemtaja waziwazi, kwa sababu ya kuwaogopa Wayahudi. 14 Hata ikawa katikati ya sikukuu Yesu alikwea kuingia hekaluni, akafundisha. 15 Wayahudi wakastaajabu wakisema, Amepataje huyu kujua elimu, ambaye hakusoma? 16 Basi Yesu akawajibu, akasema, Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka. 17 Mtu akipenda kuyatenda mapenzi yake, atajua habari ya yale mafunzo, kwamba yatoka kwa Mungu, au kwamba mimi nanena kwa nafsi yangu tu. 18 Yeye anenaye kwa nafsi yake tu hutafuta utukufu wake mwenyewe; bali yeye anayetafuta utukufu wake aliyempeleka, huyo ni wa kweli, wala ndani yake hamna udhalimu. 19 Je! Musa hakuwapa torati? Wala hakuna mmoja wenu aitendaye torati. Mbona mnatafuta kuniua? 20 Mkutano wakajibu, Ama! Una pepo! Ni nani anayetafuta kukuua? 21 Yesu akajibu, akawaambia, Mimi nalitenda kazi moja, nanyi nyote mnaistaajabia. 22 Musa aliwapa tohara; lakini si kwamba yatoka kwa Musa, bali kwa mababa; nanyi siku ya sabato humtahiri mtu. 23 Basi ikiwa mtu hupashwa tohara siku ya sabato, ili torati ya Musa isije ikavunjika, mbona mnanikasirikia mimi kwa sababu nalimfanya mtu kuwa mzima kabisa siku ya sabato? 24 Basi msihukumu hukumu ya macho tu, bali ifanyeni hukumu iliyo ya haki. 25 Basi baadhi ya watu wa Yerusalemu wakasema, Je! Huyu siye wanayemtafuta ili wamwue? 26 Na kumbe! Anena waziwazi, wala hawamwambii neno! Yamkini hao wakuu wanajua hakika ya kuwa huyu ndiye Kristo? 27 Lakini huyu twamjua atokako; bali Kristo atakapokuja hakuna ajuaye atokako. 28 Basi Yesu akapaza sauti yake hekaluni, akifundisha na kusema, Mimi mnanijua, na huko nitokako mnakujua; wala sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli, msiyemjua ninyi. 29 Mimi namjua, kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma. 30 Basi wakatafuta kumkamata; lakini hakuna mtu aliyeunyosha mkono wake ili kumshika, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado. 31 Na watu wengi katika mkutano wakamwamini; wakasema, Atakapokuja Kristo, je! Atafanya ishara nyingi zaidi kuliko hizi alizozifanya huyu? 32 Mafarisayo wakawasikia mkutano wakinung'unika hivi juu yake; basi wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakatuma watumishi ili wamkamate. 33 Basi Yesu akasema, Bado kitambo kidogo nipo pamoja nanyi; kisha naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka. 34 Mtanitafuta wala hamtaniona; nami nilipo ninyi hamwezi kuja. 35 Basi Wayahudi wakasemezana, Huyu atakwenda wapi hata sisi tusimwone? Ati! Atakwenda kwa Utawanyiko wa Wayunani, na kuwafundisha Wayunani? 36 Ni neno gani hilo alilolisema, Mtanitafuta wala hamtaniona; nami nilipo ninyi hamwezi kuja? 37 Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. 38 Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake. 39 Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa. 40 Basi wengine katika mkutano walipoyasikia maneno hayo, walisema, Hakika huyu ndiye nabii yule. 41 Wengine walisema, Huyu ndiye Kristo. Wengine wakasema, Je! Kristo atoka Galilaya? 42 Andiko halikusema ya kwamba Kristo atoka katika uzao wa Daudi, na kutoka Bethlehemu, mji ule alioukaa Daudi? 43 Basi kukaingia matengano katika mkutano kwa ajili yake. 44 Baadhi yao wakataka kumkamata, lakini hakuna mtu aliyenyosha mikono yake ili kumshika. 45 Basi wale watumishi wakawaendea wakuu wa makuhani na Mafarisayo. Nao wakawaambia, Mbona hamkumleta? 46 Wale watumishi wakajibu. Hajanena kamwe mtu ye yote kama huyu anavyonena. 47 Basi Mafarisayo wakawajibu, Je! Ninyi nanyi mmedanganyika? 48 Ni nani katika wakuu amwaminiye, au katika Mafarisayo? 49 Lakini makutano hawa wasioifahamu torati wamelaaniwa. 50 Akawaambia Nikodemo, (naye ni yule aliyemwendea zamani, maana ni mmoja wao), 51 Je! Torati yetu humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza, na kujua atendavyo? 52 Wakajibu, wakamwambia, Je! Wewe nawe umetoka Galilaya! Tafuta, ukaone ya kuwa kutoka Galilaya hakutokea nabii.

Yohana 8

1 Walikwenda kila mtu nyumbani kwake; naye Yesu akaenda mpaka mlima wa Mizeituni. 2 Hata asubuhi kulipokucha akaingia tena hekaluni, na watu wote wakamwendea; naye akaketi, akawa akiwafundisha. 3 Waandishi na Mafarisayo wakamletea mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, wakamweka katikati. 4 Wakamwambia, Mwalimu, mwanamke huyu amefumaniwa alipokuwa akizini. 5 Basi katika torati, Musa alituamuru kuwapiga kwa mawe wanawake namna hii; nawe wasemaje? 6 Nao wakasema neno hilo wakimjaribu, ili wapate sababu ya kumshitaki. Lakini Yesu akainama, akaandika kwa kidole chake katika nchi. 7 Nao walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. 8 Akainama tena, akaandika kwa kidole chake katika nchi. 9 Nao waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke amesimama katikati. 10 Yesu akajiinua asimwone mtu ila yule mwanamke, akamwambia, Mwanamke, wako wapi wale washitaki wako? Je! Hakuna aliyekuhukumu kuwa na hatia? 11 Akamwambia, Hakuna, Bwana. Yesu akamwambia, Wala mimi sikuhukumu. Enenda zako; wala usitende dhambi tena. 12 Basi Yesu akawaambia tena akasema, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima. 13 Basi Mafarisayo wakamwambia, Wewe unajishuhudia mwenyewe; ushuhuda wako si kweli. 14 Yesu akajibu, akawaambia, Mimi ningawa ninajishuhudia mwenyewe, ushuhuda wangu ndio kweli; kwa sababu najua nilikotoka na niendako; lakini ninyi hamjui nilikotoka wala niendako. 15 Ninyi mwahukumu kwa kufuata mambo ya mwili; mimi simhukumu mtu. 16 Nami nijapohukumu, hukumu yangu ni kweli; kwa kuwa mimi si peke yangu, bali ni mimi na yeye aliyenipeleka. 17 Tena katika torati yenu imeandikwa kwamba, Ushuhuda wa watu wawili ni kweli. 18 Mimi ndimi ninayejishuhudia mwenyewe, naye Baba aliyenipeleka ananishuhudia. 19 Basi wakamwambia, Yuko wapi Baba yako? Yesu akajibu, Mimi hamnijui, wala Baba yangu hammjui; kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba yangu. 20 Maneno hayo aliyasema alipokuwa akifundisha hekaluni, katika chumba cha hazina; wala hakuna mtu aliyemkamata, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado. 21 Basi akawaambia tena, Mimi naondoka, nanyi mtanitafuta; nanyi mtakufa katika dhambi yenu; mimi niendako ninyi hamwezi kuja. 22 Basi Wayahudi wakasema, Je! Atajiua! Kwa kuwa asema, Mimi niendako ninyi hamwezi kuja? 23 Akawaambia, Ninyi ni wa chini, mimi ni wa juu; ninyi ni wa ulimwengu huu, mimi si wa ulimwengu huu. 24 Kwa hiyo naliwaambieni ya kwamba mtakufa katika dhambi zenu; kwa sababu msiposadiki ya kuwa mimi ndiye, mtakufa katika dhambi zenu. 25 Basi wakamwambia, U nani wewe? Yesu akawaambia, Hasa neno lilo hilo ninalowaambia. 26 Ninayo mengi ya kusema na kuhukumu juu yenu; lakini yeye aliyenipeleka ni kweli, nami niliyoyasikia kwake, ndiyo ninenayo katika ulimwengu. 27 Wala hawakutambua ya kuwa anawatajia Baba. 28 Basi Yesu akawaambia, Mtakapokuwa mmekwisha kumwinua Mwana wa Adamu, ndipo mtakapofahamu ya kuwa mimi ndiye; na ya kuwa sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo. 29 Naye aliyenipeleka yu pamoja nami, hakuniacha peke yangu; kwa sababu nafanya sikuzote yale yampendezayo. 30 Naye alipokuwa akisema hayo, wengi walimwamini. 31 Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; 32 tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. 33 Wakamjibu, Sisi tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu wakati wo wote; nawe wasemaje, Mtawekwa huru? 34 Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. 35 Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. 36 Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli. 37 Najua ya kuwa ninyi ni uzao wa Ibrahimu lakini mnatafuta kuniua kwa sababu neno langu halimo ndani yenu. 38 Niliyoyaona kwa Baba ndiyo niyanenayo; nanyi vivyo hivyo mliyoyasikia kwa baba yenu ndiyo myatendayo. 39 Wakajibu, wakamwambia, Baba yetu ndiye Ibrahimu! Yesu akawaambia, Kama mngekuwa watoto wa Ibrahimu, mngezitenda kazi zake Ibrahimu. 40 Lakini sasa mnatafuta kuniua mimi, mtu ambaye nimewaambia iliyo kweli, niliyoisikia kwa Mungu. Ibrahimu hakufanya hivyo. 41 Ninyi mnazitenda kazi za baba yenu. Ndipo walipomwambia, Sisi hatukuzaliwa kwa zinaa; sisi tunaye Baba mmoja, yaani, Mungu. 42 Yesu akawaambia, Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi; kwa maana nalitoka kwa Mungu, nami nimekuja; wala sikuja kwa nafsi yangu, bali yeye ndiye aliyenituma. 43 Mbona hamyafahamu hayo niyasemayo? Ni kwa sababu ninyi hamwezi kulisikia neno langu. 44 Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo. 45 Nami, kwa sababu nasema iliyo kweli, hamnisadiki. 46 Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi? Nami nikisema kweli, mbona ninyi hamnisadiki? 47 Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu. 48 Wayahudi wakajibu, wakamwambia, Je! Sisi hatusemi vema ya kwamba wewe u Msamaria, nawe una pepo? 49 Yesu akajibu, Mimi sina pepo; lakini mimi namheshimu Baba yangu, na ninyi mwanivunjia heshima yangu. 50 Wala mimi siutafuti utukufu wangu; yuko mwenye kutafuta na kuhukumu. 51 Amin, amin, nawaambia, Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele. 52 Basi Wayahudi wakamwambia, Sasa tumeng'amua ya kuwa una pepo. Ibrahimu amekufa, na manabii wamekufa; nawe wasema, Mtu akilishika neno langu, hataonja mauti milele. 53 Wewe u mkuu kuliko baba yetu Ibrahimu, ambaye amekufa? Nao manabii wamekufa. Wajifanya u nani? 54 Yesu akajibu, Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu; anitukuzaye ni Baba yangu, ambaye ninyi mwanena kuwa ni Mungu wenu. 55 Wala ninyi hamkumjua; lakini mimi namjua. Nikisema ya kwamba simjui, nitakuwa mwongo kama ninyi; lakini namjua, na neno lake nalishika. 56 Ibrahimu, baba yenu, alishangilia kwa vile atakavyoiona siku yangu; naye akaiona, akafurahi. 57 Basi Wayahudi wakamwambia, Wewe hujapata bado miaka hamsini, nawe umemwona Ibrahimu? 58 Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko. 59 Basi wakaokota mawe ili wamtupie; lakini Yesu akajificha, akatoka hekaluni.

Yohana 9

1 Hata alipokuwa akipita alimwona mtu, kipofu tangu kuzaliwa. 2 Wanafunzi wake wakamwuliza wakisema, Rabi, ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu? 3 Yesu akajibu, Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake; bali kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake. 4 Imetupasa kuzifanya kazi zake yeye aliyenipeleka maadamu ni mchana, usiku waja asipoweza mtu kufanya kazi. 5 Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu. 6 Alipokwisha kusema hayo, alitema mate chini, akafanya tope kwa yale mate. Akampaka kipofu tope za macho, 7 akamwambia, Nenda kanawe katika birika ya Siloamu, (maana yake, Aliyetumwa). Basi akaenda na kunawa; akarudi anaona. 8 Basi jirani zake, na wale waliomwona zamani kuwa ni mwombaji, wakasema, Je! Huyu siye yule aliyekuwa akiketi na kuomba? 9 Wengine wakasema, Ndiye. Wengine wakasema, La, lakini amefanana naye. Yeye mwenyewe alisema, Mimi ndiye. 10 Basi wakamwambia, Macho yako yalifumbuliwaje? 11 Yeye akajibu, Mtu yule aitwaye Yesu alifanya tope, akanipaka macho akaniambia, Nenda Siloamu ukanawe; basi nikaenda na kunawa, nikapata kuona. 12 Wakamwambia, Yuko wapi huyo? Akasema, Mimi sijui. 13 Basi wakampeleka kwa Mafarisayo yule aliyekuwa kipofu zamani. 14 Nayo ilikuwa sabato, hapo Yesu alipofanya zile tope na kumfumbua macho. 15 Basi Mafarisayo nao wakamwuliza tena jinsi gani alivyopata kuona. Akawaambia, Alinitia tope juu ya macho, nami nikanawa, na sasa naona. 16 Basi baadhi ya Mafarisayo wakasema, Mtu huyo hakutoka kwa Mungu, kwa sababu haishiki sabato. Wengine wakasema, Awezaje mtu mwenye dhambi kufanya ishara kama hizo? Kukawa matengano kati yao. 17 Basi wakamwambia yule kipofu mara ya pili, Wewe wasemaje katika habari zake kwa vile alivyokufumbua macho? Akasema, Ni nabii. 18 Basi Wayahudi hawakusadiki habari zake, ya kuwa alikuwa kipofu, kisha akapata kuona; hata walipowaita wazazi wake yule aliyepata kuona. 19 Wakawauliza wakisema, Huyu ndiye mwana wenu, ambaye mnasema kwamba alizaliwa kipofu? Amepataje, basi, kuona sasa? 20 Wazazi wake wakawajibu, wakasema, Tunajua ya kuwa huyu ndiye mwana wetu, tena ya kuwa alizaliwa kipofu; 21 lakini jinsi aonavyo sasa hatujui; wala hatujui ni nani aliyemfumbua macho. Mwulizeni yeye mwenyewe; yeye ni mtu mzima; atajisemea mwenyewe. 22 Wazazi wake waliyasema hayo kwa sababu waliwaogopa Wayahudi; kwa maana Wayahudi walikuwa wamekwisha kuafikiana kwamba mtu akimkiri kuwa ni Kristo, atatengwa na sinagogi. 23 Ndiyo sababu wale wazazi wake walisema, Ni mtu mzima, mwulizeni yeye. 24 Basi mara ya pili wakamwita yule mtu aliyekuwa kipofu, wakamwambia, Mpe Mungu utukufu. Sisi tunajua ya kuwa mtu huyo ni mwenye dhambi. 25 Basi yule mtu akajibu, Kwamba yeye ni mwenye dhambi sijui. Najua neno moja, kuwa mimi nalikuwa kipofu na sasa naona. 26 Basi wakamwambia, Alikutendea nini? Alikufumbua macho jinsi gani? 27 Akawajibu, Nimekwisha kuwaambia, wala hamkusikia; mbona mnataka kusikia tena? Ninyi nanyi mnataka kuwa wanafunzi wake? 28 Basi wakamshutumu, wakasema, Wewe u mwanafunzi wake yule; sisi tu wanafunzi wa Musa. 29 Sisi tunajua ya kuwa Mungu alisema na Musa; bali yule hatujui atokako. 30 Yule mtu akajibu, akawaambia, Hii ni ajabu! Kwamba ninyi hamjui atokako, naye alinifumbua macho! 31 Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye dhambi; bali mtu akiwa ni mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake, humsikia huyo. 32 Tokea hapo haijasikiwa ya kuwa mtu ameyafumbua macho ya kipofu, ambaye alizaliwa hali hiyo. 33 Kama huyo asingalitoka kwa Mungu, asingeweza kutenda neno lo lote. 34 Wakajibu, wakamwambia, Ama! Wewe ulizaliwa katika dhambi tupu, nawe unatufundisha sisi? Wakamtoa nje. 35 Yesu akasikia kwamba wamemtoa nje; naye alipomwona alisema, Wewe wamwamini Mwana wa Mungu? 36 Naye akajibu akasema, Ni nani, Bwana, nipate kumwamini? 37 Yesu akamwambia, Umemwona, naye anayesema nawe ndiye. 38 Akasema, Naamini, Bwana. Akamsujudia. 39 Yesu akasema, Mimi nimekuja ulimwenguni humu kwa hukumu, ili wao wasioona waone, nao wanaoona wawe vipofu. 40 Baadhi ya Mafarisayo waliokuwapo pamoja naye wakasikia hayo, wakamwambia, Je! Sisi nasi tu vipofu? 41 Yesu akawaambia, Kama mngekuwa vipofu, msingekuwa na dhambi; lakini sasa mwasema, Twaona; basi dhambi yenu inakaa.

Yohana 10

1 Yesu aliwaambia, Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang'anyi. 2 Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo. 3 Bawabu humfungulia huyo, na kondoo humsikia sauti yake; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. 4 Naye awatoapo nje kondoo wake wote, huwatangulia; na wale kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake. 5 Mgeni hawatamfuata kabisa, bali watamkimbia; kwa maana hawazijui sauti za wageni. 6 Mithali hiyo Yesu aliwaambia, lakini wao hawakuelewa na mambo hayo aliyowaambia. 7 Basi Yesu aliwaambia tena, Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. 8 Wote walionitangulia ni wevi na wanyang'anyi; lakini kondoo hawakuwasikia. 9 Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho. 10 Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. 11 Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo. 12 Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwa-mwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya. 13 Yule hukimbia kwa kuwa ni mtu wa mshahara; wala mambo ya kondoo si kitu kwake. 14 Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; 15 kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo. 16 Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja. 17 Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. 18 Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu. 19 Kukaingia tena matengano kati ya Wayahudi, kwa ajili ya maneno hayo. 20 Wengi wao wakasema, Ana pepo huyu, tena ana wazimu; mbona mnamsikiliza? 21 Wengine wakasema, Maneno hayo siyo ya mtu mwenye pepo. Je! Pepo aweza kuwafumbua macho vipofu? 22 Basi huko Yerusalemu ilikuwa Sikukuu ya Kutabaruku; ni wakati wa baridi. 23 Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani. 24 Basi Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi. 25 Yesu akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia. 26 Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu. 27 Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. 28 Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. 29 Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. 30 Mimi na Baba tu umoja. 31 Basi Wayahudi wakaokota mawe tena ili wampige. 32 Yesu akawajibu, Kazi njema nyingi nimewaonyesha, zitokazo kwa Baba; kwa ajili ya kazi ipi katika hizo mnanipiga kwa mawe? 33 Wayahudi wakamjibu, Kwa ajili ya kazi njema hatukupigi kwa mawe; bali kwa kukufuru, na kwa sababu wewe uliye mwanadamu wajifanya mwenyewe u Mungu. 34 Yesu akawajibu, Je! Haikuandikwa katika torati yenu ya kwamba, Mimi nimesema, Ndinyi miungu? 35 Ikiwa aliwaita miungu wale waliojiliwa na neno la Mungu; (na maandiko hayawezi kutanguka); 36 je! Yeye ambaye Baba alimtakasa, akamtuma ulimwenguni, ninyi mnamwambia, Unakufuru; kwa sababu nalisema, Mimi ni Mwana wa Mungu? 37 Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; 38 lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba. 39 Wakatafuta tena kumkamata; lakini akatoka mikononi mwao. 40 Akaenda zake tena ng'ambo ya Yordani, mpaka mahali pale alipokuwapo Yohana akibatiza hapo kwanza, akakaa huko. 41 Na watu wengi wakamwendea, wakasema, Yohana kweli hakufanya ishara yo yote, lakini yote aliyoyasema Yohana katika habari zake huyu yalikuwa kweli. 42 Nao wengi wakamwamini huko.

Yohana 11

1 Basi mtu mmoja alikuwa hawezi, Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake. 2 Ndiye Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake, ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi. 3 Basi wale maumbu wakatuma ujumbe kwake wakisema, Bwana, yeye umpendaye hawezi. 4 Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo. 5 Naye Yesu alimpenda Martha na umbu lake na Lazaro. 6 Basi aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo. 7 Kisha, baada ya hayo, akawaambia wanafunzi wake, Twendeni Uyahudi tena. 8 Wale wanafunzi wakamwambia, Rabi, juzijuzi tu Wayahudi walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe, nawe unakwenda huko tena? 9 Yesu akajibu, Je! Saa za mchana si kumi na mbili? Mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu. 10 Bali akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake. 11 Aliyasema hayo; kisha, baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha. 12 Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona. 13 Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. 14 Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa. 15 Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake. 16 Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, Twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye. 17 Basi Yesu alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne. 18 Na Bethania ilikuwa karibu na Yerusalemu, kadiri ya maili mbili hivi; 19 na watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. 20 Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani. 21 Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. 22 Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. 23 Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. 24 Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. 25 Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; 26 naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo? 27 Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni. 28 Naye alipokwisha kusema hayo, alikwenda zake; akamwita umbu lake Mariamu faraghani, akisema, Mwalimu yupo anakuita. 29 Naye aliposikia, aliondoka upesi, akamwendea. 30 Na Yesu alikuwa hajafika ndani ya kijiji; lakini alikuwa akalipo pale pale alipomlaki Martha. 31 Basi wale Wayahudi waliokuwapo na Mariamu nyumbani, wakimfariji, walipomwona jinsi alivyoondoka upesi na kutoka, walimfuata; huku wakidhania ya kuwa anakwenda kaburini ili alie huko. 32 Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. 33 Basi Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, 34 akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. 35 Yesu akalia machozi. 36 Basi Wayahudi wakasema, Angalieni jinsi alivyompenda. 37 Bali wengine wao wakasema, Je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife? 38 Basi Yesu, hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe limewekwa juu yake. 39 Yesu akasema, Liondoeni jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne. 40 Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu? 41 Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. 42 Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. 43 Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. 44 Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake. 45 Basi wengi katika Wayahudi waliokuja kwa Mariamu, na kuyaona yale aliyoyafanya, wakamwamini. 46 Lakini wengine wakaenda zao kwa Mafarisayo, wakawaambia aliyoyafanya Yesu. 47 Basi wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakakusanya baraza, wakasema, Tunafanya nini? Maana mtu huyu afanya ishara nyingi. 48 Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu. 49 Mtu mmoja miongoni mwao, Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka ule, akawaambia, Ninyi hamjui neno lo lote; 50 wala hamfikiri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, wala lisiangamie taifa zima. 51 Na neno hilo yeye hakulisema kwa nafsi yake; bali kwa kuwa alikuwa Kuhani Mkuu mwaka ule, alitabiri ya kwamba Yesu atakufa kwa ajili ya taifa hilo. 52 Wala si kwa ajili ya taifa hilo tu; lakini pamoja na hayo awakusanye watoto wa Mungu waliotawanyika, ili wawe wamoja. 53 Basi tangu siku ile walifanya shauri la kumwua. 54 Kwa hiyo Yesu hakutembea tena kwa wazi katikati ya Wayahudi; bali alitoka huko, akaenda mahali karibu na jangwa, mpaka mji uitwao Efraimu; akakaa huko pamoja na wanafunzi wake. 55 Na Pasaka ya Wayahudi ilikuwa karibu; na wengi wakakwea toka mashambani kwenda Yerusalemu kabla ya Pasaka, ili wajitakase. 56 Basi wao wakamtafuta Yesu, wakasemezana hali wamesimama hekaluni, Mwaonaje? Haji kabisa sikukuu hii? 57 Na wakuu wa makuhani na Mafarisayo walikuwa wametoa amri ya kwamba mtu akimjua alipo, alete habari, ili wapate kumkamata.

Yohana 12

1 Basi, siku sita kabla ya Pasaka, Yesu alifika Bethania, alipokuwapo Lazaro, yeye ambaye Yesu alimfufua katika wafu. 2 Basi wakamwandalia karamu huko; naye Martha akatumikia; na Lazaro alikuwa mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja naye. 3 Basi Mariamu akatwaa ratli ya marhamu ya nardo safi yenye thamani nyingi, akampaka Yesu miguu, akamfuta miguu kwa nywele zake. Nayo nyumba pia ikajaa harufu ya marhamu. 4 Basi Yuda Iskariote, mmojawapo wa wanafunzi wake, ambaye ndiye atakaye kumsaliti, akasema, 5 Mbona marhamu hii haikuuzwa kwa dinari mia tatu, wakapewa maskini? 6 Naye aliyasema hayo, si kwa kuwahurumia maskini; bali kwa kuwa ni mwivi, naye ndiye aliyeshika mfuko, akavichukua vilivyotiwa humo. 7 Basi Yesu alisema, Mwache aiweke kwa siku ya maziko yangu. 8 Kwa maana maskini mnao sikuzote pamoja nanyi; bali mimi hamnami sikuzote. 9 Basi watu wengi katika Wayahudi walipata kujua ya kuwa yeye yuko huko, nao wakaja, si kwa ajili yake Yesu tu, ila wamwone na Lazaro, ambaye Yesu alimfufua katika wafu. 10 Nao wakuu wa makuhani wakafanya shauri la kumwua Lazaro naye; 11 maana kwa ajili yake wengi katika Wayahudi walijitenga, wakamwamini Yesu. 12 Nayo siku ya pili yake watu wengi walioijia sikukuu walisikia ya kwamba Yesu anakuja Yerusalemu; 13 wakatwaa matawi ya mitende, wakatoka nje kwenda kumlaki, wakapiga makelele, Hosana! Ndiye mbarikiwa ajaye kwa jina la Bwana, Mfalme wa Israeli! 14 Naye Yesu alikuwa amepata mwana-punda, akampanda, kama vile iliyoandikwa, 15 Usiogope, binti Sayuni; tazama, Mfalme wako anakuja, amepanda mwana-punda. 16 Mambo hayo wanafunzi wake hawakuyafahamu hapo kwanza; lakini Yesu alipotukuzwa, ndipo walipokumbuka ya kwamba ameandikiwa hayo, na ya kwamba walimtendea hayo. 17 Basi wakamshuhudia wale mkutano waliokuwapo pamoja naye alipomwita Lazaro kutoka kaburini, akamfufua. 18 Na kwa sababu hiyo mkutano walikwenda kumlaki, kwa kuwa wamesikia ya kwamba ameifanya ishara hiyo. 19 Basi Mafarisayo wakasemezana wao kwa wao, Mwaona kwamba hamfai neno lo lote; tazameni, ulimwengu umekwenda nyuma yake. 20 Palikuwa na Wayunani kadha wa kadha miongoni mwa watu waliokwea kwenda kuabudu kwenye sikukuu. 21 Basi hao walimwendea Filipo, mtu wa Bethsaida ya Galilaya, wakamwomba, wakisema, Bwana, sisi tunataka kumwona Yesu. 22 Filipo akaenda, akamwambia Andrea; kisha Andrea na Filipo wakamwambia Yesu. 23 Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. 24 Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. 25 Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. 26 Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu. 27 Sasa roho yangu imefadhaika; nami nisemeje? Baba, uniokoe katika saa hii? Lakini ni kwa ajili ya hayo nilivyoifikia saa hii. 28 Baba, ulitukuze jina lako. Basi ikaja sauti kutoka mbinguni, Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena. 29 Basi mkutano uliosimama karibu wakasikia, walisema ya kwamba kumekuwa ngurumo; wengine walisema, Malaika amesema naye. 30 Yesu akajibu, akasema, Sauti hiyo haikuwako kwa ajili yangu, bali kwa ajili yenu. 31 Sasa hukumu ya ulimwengu huu ipo; sasa mkuu wa ulimwengu huu atatupwa nje. 32 Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu. 33 Aliyanena hayo akionyesha ni mauti gani atakayokufa. 34 Basi mkutano wakamjibu, Sisi tumesikia katika torati ya kwamba Kristo adumu hata milele; nawe wasemaje ya kwamba imempasa Mwana wa Adamu kuinuliwa? Huyu Mwana wa Adamu ni nani? 35 Basi Yesu akawaambia, Nuru ingaliko pamoja nanyi muda kidogo. Enendeni maadamu mnayo nuru hiyo, giza lisije likawaweza; maana aendaye gizani hajui aendako. 36 Maadamu mnayo nuru, iaminini nuru hiyo, ili mpate kuwa wana wa nuru. Hayo aliyasema Yesu, akaenda zake, akajificha wasimwone. 37 Walakini ajapokuwa amefanya ishara nyingi namna hiyo mbele yao, hawakumwamini; 38 ili litimie lile neno la nabii Isaya alilolisema, Bwana, ni nani aliyezisadiki habari zetu; Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani? 39 Ndiyo sababu wao hawakuweza kusadiki; kwa maana Isaya alisema tena, 40 Amewapofusha macho, Ameifanya mizito mioyo yao; Wasije wakaona kwa macho yao, Wakafahamu kwa mioyo yao, Wakaongoka, nikawaponya. 41 Maneno hayo aliyasema Isaya, kwa kuwa aliuona utukufu wake, akataja habari zake. 42 Walakini hata katika wakuu walikuwamo wengi waliomwamini; lakini kwa sababu ya Mafarisayo hawakumkiri, wasije wakatengwa na sinagogi. 43 Kwa maana walipenda utukufu wa wanadamu kuliko utukufu wa Mungu. 44 Naye Yesu akapaza sauti, akasema, Yeye aniaminiye mimi, haniamini mimi bali yeye aliyenipeleka. 45 Naye anitazamaye mimi amtazama yeye aliyenipeleka. 46 Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani. 47 Na mtu akiyasikia maneno yangu, asiyashike, mimi simhukumu; maana sikuja ili niuhukumu ulimwengu, ila niuokoe ulimwengu. 48 Yeye anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, anaye amhukumuye; neno hilo nililolinena ndilo litakalomhukumu siku ya mwisho. 49 Kwa sababu mimi sikunena kwa nafsi yangu tu; bali Baba aliyenipeleka, yeye mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema. 50 Nami najua ya kuwa agizo lake ni uzima wa milele; basi hayo ninenayo mimi, kama Baba alivyoniambia, ndivyo ninenavyo.

Yohana 13

1 Basi, kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo. 2 Hata wakati wa chakula cha jioni; naye Ibilisi amekwisha kumtia Yuda, mwana wa Simoni Iskariote, moyo wa kumsaliti; 3 Yesu, hali akijua ya kuwa Baba amempa vyote mikononi mwake, na ya kuwa alitoka kwa Mungu naye anakwenda kwa Mungu, 4 aliondoka chakulani; akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. 5 Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga. 6 Hivyo yuaja kwa Simoni Petro. Huyo akamwambia, Bwana! Wewe wanitawadha miguu mimi? 7 Yesu akajibu, akamwambia, Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye. 8 Petro akamwambia, Wewe hutanitawadha miguu kamwe. Yesu akamwambia, Kama nisipokutawadha, huna shirika nami. 9 Simoni Petro akamwambia, Bwana, si miguu yangu tu, hata na mikono yangu na kichwa changu pia. 10 Yesu akamwambia, Yeye aliyekwisha kuoga hana haja ila ya kutawadha miguu, bali yu safi mwili wote; nanyi mmekuwa safi, lakini si nyote. 11 Kwa maana alimjua yeye atakayemsaliti; ndiyo maana alisema, Si nyote mlio safi. 12 Basi alipokwisha kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea? 13 Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. 14 Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi. 15 Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo. 16 Amin, amin, nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka. 17 Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda. 18 Sisemi habari za ninyi nyote; nawajua wale niliowachagua; lakini andiko lipate kutimizwa, Aliyekula chakula changu Ameniinulia kisigino chake. 19 Tangu sasa nawaambia kabla hayajatukia, ili yatakapotukia mpate kuamini ya kuwa mimi ndiye. 20 Amin, amin, nawaambieni, Yeye ampokeaye mtu ye yote nimpelekaye, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi; ampokea yeye aliyenipeleka. 21 Naye alipokwisha kusema hayo, Yesu alifadhaika rohoni, akashuhudia akisema, Amin, amin, nawaambieni, Mmoja wenu atanisaliti. 22 Wanafunzi wakatazamana, huku wakiona shaka ni nani amtajaye. 23 Na palikuwapo mmoja wa wanafunzi wake, ameegama kifuani pa Yesu, ambaye Yesu alimpenda. 24 Basi Simoni Petro akampungia mkono, akamwambia, Uliza, ni nani amtajaye? 25 Basi yeye, hali akimwelekea Yesu kifua chake, akamwambia, Bwana, ni nani? 26 Basi Yesu akajibu, Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa. Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. 27 Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, Uyatendayo yatende upesi. 28 Wala hakuna mtu katika wale walioketi chakulani aliyeijua sababu ya kumwambia hivyo. 29 Kwa maana wengine walidhania, kwa kuwa Yuda huchukua mfuko, ya kwamba Yesu alimwambia kama, Nunua mnavyovihitaji kwa sikukuu; au kwamba awape maskini kitu. 30 Basi huyo, akiisha kulipokea lile tonge, akatoka mara hiyo. Nako kulikuwa ni usiku. 31 Basi huyo alipokwisha kutoka, Yesu alisema, Sasa ametukuzwa Mwana wa Adamu, naye Mungu ametukuzwa ndani yake. 32 Mungu naye atamtukuza ndani ya nafsi yake; naye atamtukuza mara. 33 Enyi watoto wadogo, bado kitambo kidogo nipo pamoja nanyi; mtanitafuta; na kama vile nilivyowaambia Wayahudi ya kwamba, Mimi niendako ninyi hamwezi kuja; kadhalika sasa nawaambia ninyi. 34 Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. 35 Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi. 36 Simoni Petro akamwambia, Bwana, unakwendapi? Yesu akamjibu, Niendako huwezi kunifuata sasa; lakini utanifuata baadaye. 37 Petro akamwambia, Bwana, kwa nini mimi nisiweze kukufuata sasa? Mimi nitautoa uhai wangu kwa ajili yako. 38 Yesu akamjibu, Je! Wewe utautoa uhai wako kwa ajili yangu? Amin, amin, nakuambia, Jimbi hatawika hata wewe utakapokuwa umenikana mara tatu.

Yohana 14

1 Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. 2 Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. 3 Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo. 4 Nami niendako mwaijua njia. 5 Tomaso akamwambia, Bwana, sisi hatujui uendako; nasi twaijuaje njia? 6 Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. 7 Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba; tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. 8 Filipo akamwambia, Bwana, utuonyeshe Baba, yatutosha. 9 Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje, Utuonyeshe Baba? 10 Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake. 11 Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! Hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe. 12 Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba. 13 Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana. 14 Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya. 15 Mkinipenda, mtazishika amri zangu. 16 Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; 17 ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu. 18 Sitawaacha ninyi yatima; naja kwenu. 19 Bado kitambo kidogo na ulimwengu haunioni tena; bali ninyi mnaniona. Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi nanyi mtakuwa hai. 20 Siku ile ninyi mtatambua ya kuwa mimi ni ndani ya Baba yangu, nanyi ndani yangu, nami ndani yenu. 21 Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake. 22 Yuda (siye Iskariote), akamwambia, Bwana, imekuwaje ya kwamba wataka kujidhihirisha kwetu, wala si kwa ulimwengu? 23 Yesu akajibu, akamwambia, Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake. 24 Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka. 25 Hayo ndiyo niliyowaambia wakati nilipokuwa nikikaa kwenu. 26 Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia. 27 Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga. 28 Mlisikia ya kwamba mimi naliwaambia, Naenda zangu, tena naja kwenu. Kama mngalinipenda, mngalifurahi kwa sababu naenda kwa Baba, kwa maana Baba ni mkuu kuliko mimi. 29 Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. 30 Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu. 31 Lakini ulimwengu ujue ya kuwa nampenda Baba; na kama vile Baba alivyoniamuru; ndivyo nifanyavyo. Ondokeni, twendeni zetu.

Yohana 15

1 Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. 2 Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa. 3 Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia. 4 Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. 5 Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote. 6 Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea. 7 Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa. 8 Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu. 9 Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu. 10 Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. 11 Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe. 12 Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi. 13 Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. 14 Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo. 15 Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu. 16 Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni. 17 Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana. 18 Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. 19 Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. 20 Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu. 21 Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka. 22 Kama nisingalikuja na kusema nao, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa hawana udhuru kwa dhambi yao. 23 Yeye anichukiaye mimi humchukia na Baba yangu. 24 Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. 25 Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure. 26 Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia. 27 Nanyi pia mnashuhudia, kwa kuwa tangu mwanzo mmekuwapo pamoja nami.

Yohana 16

1 Maneno hayo nimewaambia, msije mkachukizwa. 2 Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada. 3 Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi. 4 Lakini nimewaambia hayo, ili makusudi saa ile itakapokuja myakumbuke ya kuwa mimi naliwaambia. Sikuwaambia hayo tangu mwanzo, kwa sababu nalikuwapo pamoja nanyi. 5 Lakini sasa mimi naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka, wala hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi? 6 Ila kwa sababu nimewaambia hayo huzuni imejaa mioyoni mwenu. 7 Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. 8 Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu. 9 Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi; 10 kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena; 11 kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha kuhukumiwa. 12 Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. 13 Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake. 14 Yeye atanitukuza mimi, kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari. 15 Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari. 16 Bado kitambo kidogo nanyi hamnioni; na tena bado kitambo kidogo nanyi mtaniona. 17 Basi baadhi ya wanafunzi wake wakasemezana, Neno gani hilo asemalo, Bado kitambo kidogo nanyi hamnioni, na tena bado kitambo kidogo nanyi mtaniona? Na hilo, Kwa sababu naenda zangu kwa Baba? 18 Basi walisema, Neno gani hilo asemalo; hilo, Bado kitambo kidogo? Hatujui asemalo. 19 Yesu alifahamu ya kwamba wanataka kumwuliza, akawaambia, Ndilo hilo mnaloulizana, ya kuwa nalisema, Bado kitambo kidogo nanyi hamnioni, na tena bado kitambo kidogo nanyi mtaniona? 20 Amin, amin, nawaambia, Ninyi mtalia na kuomboleza, bali ulimwengu utafurahi; ninyi mtahuzunishwa, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha. 21 Mwanamke azaapo, yuna huzuni kwa kuwa saa yake imefika; lakini akiisha kuzaa mwana, haikumbuki tena ile dhiki, kwa sababu ya furaha ya kuzaliwa mtu ulimwenguni. 22 Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye. 23 Tena siku ile hamtaniuliza neno lo lote. Amin, amin, nawaambia, Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu. 24 Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu. 25 Hayo nimesema nanyi kwa mithali; saa yaja ambapo sitasema nanyi tena kwa mithali, lakini nitawapa waziwazi habari ya Baba. 26 Na siku ile mtaomba kwa jina langu, wala siwaambii ya kwamba mimi nitawaombea kwa Baba; 27 kwa maana Baba mwenyewe awapenda kwa kuwa ninyi mmenipenda mimi, na kusadiki ya kwamba mimi nalitoka kwa Baba. 28 Nalitoka kwa Baba, nami nimekuja hapa ulimwenguni; tena nauacha ulimwengu; na kwenda kwa Baba. 29 Basi wanafunzi wake wakasema, Tazama, sasa wasema waziwazi, wala huneni mithali yo yote. 30 Sasa tumejua ya kuwa wewe wafahamu mambo yote, wala huna haja ya mtu akuulize; kwa hiyo twasadiki ya kwamba ulitoka kwa Mungu. 31 Yesu akawajibu, Je! Mnasadiki sasa? 32 Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami. 33 Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.

Yohana 17

1 Maneno hayo aliyasema Yesu; akainua macho yake kuelekea mbinguni, akasema, Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe; 2 kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. 3 Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma. 4 Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye. 5 Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako. 6 Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu; walikuwa wako, ukanipa mimi, na neno lako wamelishika. 7 Sasa wamejua ya kuwa yote uliyonipa yatoka kwako. 8 Kwa kuwa maneno uliyonipa nimewapa wao; nao wakayapokea, wakajua hakika ya kuwa nalitoka kwako, wakasadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. 9 Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako; 10 na wote walio wangu ni wako, na walio wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao. 11 Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba mtakatifu, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo. 12 Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie. 13 Na sasa naja kwako; na maneno haya nayasema ulimwenguni, ili wawe na furaha yangu imetimizwa ndani yao. 14 Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. 15 Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. 16 Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. 17 Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. 18 Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni. 19 Na kwa ajili yao najiweka wakfu mwenyewe, ili na hao watakaswe katika kweli. 20 Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao. 21 Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. 22 Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja. 23 Mimi ndani yao, nawe ndani yangu, ili wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma, ukawapenda wao kama ulivyonipenda mimi. 24 Baba, hao ulionipa nataka wawe pamoja nami po pote nilipo, wapate na kuutazama utukufu wangu ulionipa; kwa maana ulinipenda kabla ya kuwekwa msingi ulimwengu. 25 Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua; lakini mimi nalikujua, na hao wamejua ya kuwa ndiwe uliyenituma. 26 Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao.

Yohana 18

1 Alipokwisha kusema hayo, Yesu alitoka pamoja na wanafunzi wake kwenda ng'ambo ya kijito Kedroni, palipokuwapo bustani; akaingia yeye na wanafunzi wake. 2 Naye Yuda, yule aliyetaka kumsaliti, alipajua mahali pale; kwa sababu Yesu alikuwa akienda huko mara nyingi pamoja na wanafunzi wake. 3 Basi Yuda, akiisha kupokea kikosi cha askari na watumishi waliotoka kwa wakuu wa makuhani na Mafarisayo, akaenda huko na taa na mienge na silaha. 4 Basi Yesu, hali akijua yote yatakayompata, akatokea, akawaambia, Ni nani mnayemtafuta? 5 Wao wakamjibu, Ni Yesu Mnazareti. Yesu akawaambia, Ni mimi. Yuda naye aliyemsaliti alikuwa amesimama pamoja nao. 6 Basi alipowaambia, Ni mimi, walirudi nyuma, wakaanguka chini. 7 Basi akawauliza tena, Mnamtafuta nani? Wakasema, Yesu Mnazareti. 8 Yesu akajibu, Nimekwisha kuwaambieni ya kwamba ni mimi; basi ikiwa mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao. 9 Ili litimizwe lile neno alilolisema, Wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja wao. 10 Basi Simoni Petro alikuwa na upanga, akaufuta, akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio la kuume. Na yule mtumwa jina lake ni Malko. 11 Basi Yesu akamwambia Petro, Rudisha upanga alani mwake; je! Kikombe alichonipa Baba, mimi nisikinywee? 12 Basi wale askari na yule jemadari na wale watumishi wa Wayahudi walimkamata Yesu, wakamfunga. 13 Wakamchukua kwa Anasi kwanza; maana alikuwa mkwewe Kayafa, yule aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka ule. 14 Naye Kayafa ndiye yule aliyewapa Wayahudi lile shauri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu. 15 Wakamfuata Yesu, Petro na mwanafunzi mwingine. Na mwanafunzi huyo alikuwa amejulikana na Kuhani Mkuu, akaingia pamoja na Yesu katika behewa ya Kuhani Mkuu. 16 Lakini Petro akasimama nje mlangoni. Basi yule mwanafunzi mwingine aliyejulikana na Kuhani Mkuu akatoka, akasema na mngoja mlango, akamleta Petro ndani. 17 Basi yule kijakazi, aliyekuwa mngoja mlango, akamwambia Petro, Wewe nawe, je! Hu mwanafunzi mmojawapo wa mtu huyu? Naye akasema, Si mimi. 18 Na wale watumwa na watumishi walikuwa wakisimama, wamefanya moto wa makaa; maana ilikuwa baridi; wakawa wakikota moto. Petro naye alikuwapo pamoja nao, anakota moto. 19 Basi Kuhani Mkuu akamwuliza Yesu habari za wanafunzi wake, na habari za mafundisho yake. 20 Yesu akamjibu, Mimi nimesema na ulimwengu waziwazi; sikuzote nalifundisha katika sinagogi na katika hekalu, wakusanyikapo Wayahudi wote; wala kwa siri mimi sikusema neno lo lote. 21 Ya nini kuniuliza mimi? Waulize wale waliosikia ni nini niliyowaambia; wao wanajua niliyoyanena. 22 Basi aliposema hayo, mtumishi mmojawapo aliyesimama karibu alimpiga Yesu kofi akisema, Wamjibu hivi Kuhani Mkuu? 23 Yesu akamjibu, Kama nimesema vibaya, ushuhudie ule ubaya; bali kama nimesema vema, wanipigia nini? 24 Basi Anasi akampeleka hali amefungwa kwa Kayafa, Kuhani Mkuu. 25 Na Simoni Petro alikuwa akisimama huko, anakota moto. Basi wakamwambia, Wewe nawe, je! Hu mwanafunzi wake mmojawapo? Naye akakana, akasema, Si mimi. 26 Mtumwa mmojawapo wa Kuhani Mkuu, naye ni jamaa yake yule aliyekatwa sikio na Petro, akasema, Je! Mimi sikukuona wewe bustanini pamoja naye? 27 Basi Petro akakana tena, na mara akawika jimbi. 28 Kisha wakamchukua Yesu kutoka kwa Kayafa mpaka Praitorio, nayo ikawa alfajiri;lakini wao wenyewe hawakuingia ndani ya ile praitorio,wasije wakanajisika,bali wapate kuila Pasaka. 29 Basi Pilato akawatokea nje, akasema, Ni mashitaka gani mnayoleta juu ya mtu huyu? 30 Wakajibu, wakamwambia, Kama huyu asingekuwa mtenda mabaya, tusingemleta kwako. 31 Basi Pilato akawaambia, Haya! Mtwaeni ninyi, mkamhukumu kwa ile torati yenu! Wayahudi wakamwambia, Sisi hatuna ruhusa ya kuua mtu. 32 Ili litimie lile neno lake Yesu alilolisema, akionyesha ni mauti gani atakayokufa. 33 Basi Pilato akaingia tena ndani ya Praitorio, akamwita Yesu, akamwambia, Je! Wewe ni Mfalme wa Wayahudi? 34 Yesu akamjibu, Wewe wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine walikuambia habari zangu? 35 Pilato akajibu, Ama! Ni Myahudi mimi! Taifa lako na wakuu wa makuhani ndio waliokuleta kwangu. Umefanya nini? 36 Yesu akajibu, Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa. 37 Basi Pilato akamwambia, Wewe u mfalme basi? Yesu akajibu, Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu. 38 Pilato akamwambia, Kweli ni nini? Naye akiisha kusema neno hilo akawatokea Wayahudi tena, akawaambia, Mimi sioni hatia yo yote kwake. 39 Lakini kwenu kuna desturi ya mimi kuwafungulia mtu mmoja wakati wa Pasaka; basi, mwapenda niwafungulie Mfalme wa Wayahudi? 40 Basi wakapiga kelele tena kusema, Si huyu, bali Baraba. Naye yule Baraba alikuwa mnyang'anyi.

Yohana 19

1 Basi ndipo Pilato alipomtwaa Yesu, akampiga mijeledi. 2 Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika vazi la zambarau. 3 Wakawa wakimwendea, wakisema, Salamu! Mfalme wa Wayahudi! Wakampiga makofi. 4 Kisha Pilato akatokea tena nje, akawaambia, Mtu huyu namleta nje kwenu, mpate kufahamu ya kuwa mimi sioni hatia yo yote kwake. 5 Ndipo Yesu alipotoka nje, naye amevaa ile taji ya miiba, na lile vazi la zambarau. Pilato akawaambia, Tazama, mtu huyu! 6 Basi wale wakuu wa makuhani na watumishi wao walipomwona, walipiga kelele wakisema, Msulibishe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Mtwaeni ninyi basi, mkamsulibishe; kwa maana mimi sioni hatia kwake. 7 Wayahudi wakamjibu, Sisi tunayo sheria, na kwa sheria hiyo amestahili kufa, kwa sababu alijifanya kuwa Mwana wa Mungu. 8 Basi Pilato aliposikia neno hilo, akazidi kuogopa. 9 Akaingia tena ndani ya ile Praitorio, akamwambia Yesu, Wewe umetokapi? Lakini Yesu hakumpa jibu lo lote. 10 Basi Pilato akamwambia, Husemi nami? Hujui ya kuwa mimi nina mamlaka ya kukufungua, nami nina mamlaka ya kukusulibisha? 11 Yesu akamjibu, Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo yeye aliyenitia mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi. 12 Na tangu hapo Pilato akatafuta kumfungua; lakini Wayahudi wakapiga makelele wakisema, Ukimfungua huyu, wewe si rafiki yake Kaisari; kila mtu ajifanyaye kuwa mfalme humfitini Kaisari. 13 Basi Pilato, aliposikia maneno hayo, akamleta Yesu nje, akaketi juu ya kiti cha hukumu, mahali paitwapo Sakafu ya Mawe, au kwa Kiebrania, Gabatha. 14 Nayo ilikuwa Maandalio ya pasaka, yapata saa sita. Akawaambia Wayahudi, Tazama, Mfalme wenu! 15 Basi wale wakapiga kelele, Mwondoshe! Mwondoshe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Je! Nimsulibishe mfalme wenu! Wakuu wa makuhani wakamjibu, Sisi hatuna mfalme ila Kaisari. 16 Basi ndipo alipomtia mikononi mwao ili asulibiwe; nao wakampokea Yesu. 17 Akatoka, hali akijichukulia msalaba wake, mpaka mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, au kwa Kiebrania, Golgotha. 18 Wakamsulibisha huko, na wengine wawili pamoja naye, mmoja huku na mmoja huku, na Yesu katikati. 19 Naye Pilato akaandika anwani, akaiweka juu ya msalaba, imeandikwa, YESU MNAZARETI, MFALME WA WAYAHUDI. 20 Basi anwani hiyo waliisoma wengi katika Wayahudi; maana mahali pale aliposulibiwa Yesu palikuwa karibu na mji; nayo iliandikwa kwa Kiebrania, na Kirumi, na Kiyunani. 21 Basi wakuu wa makuhani na Wayahudi wakamwambia Pilato, Usiandike, Mfalme wa Wayahudi; bali ya kwamba yule alisema, Mimi ni mfalme wa Wayahudi. 22 Pilato akajibu, Niliyoandika nimeyaandika. 23 Nao askari walipomsulibisha Yesu, waliyatwaa mavazi yake, wakafanya mafungu manne, kwa kila askari fungu lake; na kanzu nayo. Basi kanzu ile haikushonwa, ilikuwa imefumwa yote pia tangu juu. 24 Basi wakaambiana, Tusiipasue, lakini tuipigie kura, iwe ya nani. Ili litimie andiko lile linenalo, Waligawanya nguo zangu, Na vazi langu wakalipigia kura. Basi ndivyo walivyofanya wale askari. 25 Na penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. 26 Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. 27 Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake. 28 Baada ya hayo Yesu, hali akijua ya kuwa yote yamekwisha kumalizika ili andiko litimizwe, akasema, Naona kiu. 29 Kulikuwako huko chombo kimejaa siki; basi wakatia sifongo iliyojaa siki juu ya ufito wa hisopo, wakampelekea kinywani. 30 Basi Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, Imekwisha. Akainama kichwa, akaisalimu roho yake. 31 Basi Wayahudi, kwa sababu ni Maandalio, miili isikae juu ya misalaba siku ya sabato, (maana sabato ile ilikuwa siku kubwa), walimwomba Pilato miguu yao ivunjwe, wakaondolewe. 32 Basi askari wakaenda, wakamvunja miguu wa kwanza, na wa pili, aliyesulibiwa pamoja naye. 33 Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu; 34 lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji. 35 Naye aliyeona ameshuhudia, na ushuhuda wake ni kweli; naye anajua ya kuwa anasema kweli ili ninyi nanyi mpate kusadiki. 36 Kwa maana hayo yalitukia ili andiko litimie, Hapana mfupa wake utakaovunjwa. 37 Na tena andiko lingine lanena, Watamtazama yeye waliyemchoma. 38 Hata baada ya hayo Yusufu wa Arimathaya, naye ni mwanafunzi wa Yesu, (lakini kwa siri, kwa hofu ya Wayahudi), alimwomba Pilato ruhusa ili auondoe mwili wake Yesu. Na Pilato akampa ruhusa. Basi akaenda, akauondoa mwili wake. 39 Akaenda Nikodemo naye, (yule aliyemwendea usiku hapo kwanza), akaleta machanganyiko ya manemane na uudi, yapata ratli mia. 40 Basi wakautwaa mwili wake Yesu, wakaufunga sanda ya kitani pamoja na yale manukato, kama ilivyo desturi ya Wayahudi katika kuzika. 41 Na pale pale aliposulibiwa palikuwa na bustani; na ndani ya bustani mna kaburi jipya, ambalo hajatiwa bado mtu ye yote ndani yake. 42 Humo basi, kwa sababu ya Maandalio ya Wayahudi, wakamweka Yesu; maana lile kaburi lilikuwa karibu.

Yohana 20

1 Hata siku ya kwanza ya juma Mariamu Magdalene alikwenda kaburini alfajiri, kungali giza bado; akaliona lile jiwe limeondolewa kaburini. 2 Basi akaenda mbio, akafika kwa Simoni Petro na kwa yule mwanafunzi mwingine ambaye Yesu alimpenda, akawaambia, Wamemwondoa Bwana kaburini, wala hatujui walikomweka. 3 Basi Petro akatoka, na yule mwanafunzi mwingine, wakashika njia kwenda kaburini. 4 Wakaenda mbio wote wawili; na yule mwanafunzi mwingine akaenda mbio upesi kuliko Petro, akawa wa kwanza kufika kaburini. 5 Akainama na kuchungulia, akaona vitambaa vya sanda vimelala; lakini hakuingia. 6 Basi akaja na Simoni Petro, akaingia ndani ya kaburi; akavitazama vitambaa vilivyolala, 7 na ile leso iliyokuwako kichwani pake; haikulala pamoja na vitambaa, bali imezongwa-zongwa mbali mahali pa peke yake. 8 Basi ndipo alipoingia naye yule mwanafunzi mwingine aliyekuwa wa kwanza wa kufika kaburini, akaona na kuamini. 9 Kwa maana hawajalifahamu bado andiko, ya kwamba imempasa kufufuka. 10 Basi wale wanafunzi wakaenda zao tena nyumbani kwao. 11 Lakini Mariamu alikuwa akisimama karibu na kaburi, nje yake, analia. Basi akilia hivi, aliinama na kuchungulia ndani ya kaburi. 12 Akaona malaika wawili, wenye mavazi meupe, wameketi, mmoja kichwani na mmoja miguuni, hapo ulipolazwa mwili wake Yesu. 13 Nao wakamwambia, Mama, unalilia nini? Akawaambia, Kwa sababu wamemwondoa Bwana wangu, wala mimi sijui walikomweka. 14 Naye akiisha kusema hayo, akageuka nyuma, akamwona Yesu amesimama, asijue ya kuwa ni Yesu. 15 Yesu akamwambia, Mama, unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa. 16 Yesu akamwambia, Mariamu. Yeye akageuka, akamwambia kwa Kiebrania, Raboni! (Yaani, Mwalimu wangu). 17 Yesu akamwambia. Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu. 18 Mariamu Magdalene akaenda, akawapasha wanafunzi habari ya kwamba, Nimemwona Bwana, na ya kwamba amemwambia hayo. 19 Ikawa jioni, siku ile ya kwanza ya juma, pale walipokuwapo wanafunzi, milango imefungwa kwa hofu ya Wayahudi; akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu. 20 Naye akiisha kusema hayo, akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana. 21 Basi Yesu akawaambia tena, Amani iwe kwenu; kama Baba alivyonituma mimi, mimi nami nawapeleka ninyi. 22 Naye akiisha kusema hayo, akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu. 23 Wo wote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa. 24 Walakini mmoja wa wale Thenashara, Tomaso, aitwaye Pacha, hakuwako pamoja nao alipokuja Yesu. 25 Basi wanafunzi wengine wakamwambia, Tumemwona Bwana. Akawaambia, Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo. 26 Basi, baada ya siku nane, wanafunzi wake walikuwamo ndani tena, na Tomaso pamoja nao. Akaja Yesu, na milango imefungwa, akasimama katikati, akasema, Amani iwe kwenu. 27 Kisha akamwambia Tomaso, Lete hapa kidole chako; uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala usiwe asiyeamini, bali aaminiye. 28 Tomaso akajibu, akamwambia, Bwana wangu na Mungu wangu! 29 Yesu akamwambia, Wewe, kwa kuwa umeniona, umesadiki; wa heri wale wasioona, wakasadiki. 30 Basi kuna ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake, zisizoandikwa katika kitabu hiki. 31 Lakini hizi zimeandikwa ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe na uzima kwa jina lake.

Yohana 21

1 Baada ya hayo Yesu alijidhihirisha tena kwa wanafunzi wake, penye bahari ya Tiberia, naye alijidhihirisha hivi. 2 Simoni Petro, na Tomaso aitwaye Pacha, na Nathanaeli wa Kana ya Galilaya, na wana wa Zebedayo, na wengine wawili wa wanafunzi wake, walikuwapo pamoja. 3 Simoni Petro aliwaambia, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu. 4 Hata asubuhi kulipokucha, Yesu alisimama ufuoni; walakini wanafunzi hawakujua ya kuwa ni Yesu. 5 Basi Yesu akawaambia, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La. 6 Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki. 7 Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana. Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini. 8 Na hao wanafunzi wengine wakaja katika mashua; maana hawakuwa mbali na nchi kavu; ila yapata dhiraa mia mbili; huku wakilikokota lile jarife lenye samaki. 9 Basi waliposhuka pwani, wakaona huko moto wa makaa, na juu yake pametiwa samaki, na mkate. 10 Yesu akawaambia, Leteni hapa baadhi ya samaki mliowavua sasa hivi. 11 Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka. 12 Yesu akawaambia, Njoni mfungue kinywa. Wala hakuna mtu katika wale wanafunzi aliyethubutu kumwuliza, U nani wewe? Wakijua ya kuwa ni Bwana. 13 Yesu akaenda akautwaa mkate, akawapa, na samaki vivyo hivyo. 14 Hiyo ndiyo mara ya tatu ya Yesu kuonekana na wanafunzi wake baada ya kufufuka katika wafu. 15 Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam,Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. 16 Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. 17 Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu. 18 Akasema, Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka. 19 Akasema neno hilo kwa kuonyesha ni kwa mauti gani atakayomtukuza Mungu. Naye akiisha kusema hayo akamwambia, Nifuate. 20 Petro akageuka akamwona yule mwanafunzi aliyependwa na Yesu anafuata; (ndiye huyo aliyeegama kifuani pake wakati wa kula chakula cha jioni, akasema, Bwana, ni nani akusalitiye?) 21 Basi Petro akamwona huyo, akamwambia Yesu, Bwana, na huyu je? 22 Yesu akamwambia, Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? Wewe unifuate mimi. 23 Basi neno hilo lilienea katikati ya ndugu ya kwamba mwanafunzi yule hafi. Walakini Yesu hakumwambia ya kwamba hafi; bali, Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? 24 Huyu ndiye yule mwanafunzi ayashuhudiaye haya, na aliyeyaandika haya: nasi twajua ya kuwa ushuhuda wake ni kweli. 25 Kuna na mambo mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa.

Matendo ya Mitume 1

1 Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, 2 hata siku ile alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa Roho Mtakatifu wale mitume aliowachagua; 3 wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. 4 Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; 5 ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache. 6 Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? 7 Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. 8 Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi. 9 Akiisha kusema hayo, walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao. 10 Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe, 11 wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni. 12 Kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato. 13 Hata walipoingia, wakapanda orofani, walipokuwa wakikaa; Petro, na Yohana, na Yakobo, na Andrea, Filipo na Tomaso, Bartholomayo na Mathayo, Yakobo wa Alfayo, na Simoni Zelote, na Yuda wa Yakobo. 14 Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake, na Mariamu mama yake Yesu, na ndugu zake. 15 Siku zile akasimama Petro kati ya hao ndugu (jumla ya majina ilipata mia na ishirini), akasema, 16 Ndugu, ilipasa andiko litimizwe, alilolinena Roho Mtakatifu zamani kwa kinywa cha Daudi, katika habari za Yuda aliyewaongoza wao waliomkamata Yesu; 17 kwa sababu alikuwa amehesabiwa pamoja na sisi, akapata sehemu ya huduma hii. 18 (Basi mtu huyu alinunua konde kwa ijara ya udhalimu; akaanguka kwa kasi akapasuka matumbo yake yote yakatoka. 19 Ikajulikana na watu wote wakaao Yerusalemu; hata konde lile likaitwa kwa lugha yao Akeldama, maana yake, konde la damu.) 20 Kwa maana imeandikwa katika chuo cha Zaburi, Kikao chake na kiwe ukiwa, Wala asiwepo mtu mwenye kukaa humo; 21 Basi katika watu waliofuatana nasi wakati wote Bwana Yesu alipokuwa akiingia na kutoka kwetu, 22 kuanza tangu ubatizo wa Yohana, hata siku ile alipochukuliwa kwetu kwenda juu, inapasa mmoja wao awe shahidi wa kufufuka kwake pamoja nasi. 23 Wakaweka wawili, Yusufu, aitwaye Barsaba, aliyekuwa na jina la pili Yusto, na Mathiya. 24 Kisha wakaomba, wakasema, Wewe, Bwana, ujuaye mioyo ya watu wote, tuonyeshe ni nani uliyemchagua katika hawa wawili, 25 ashike mahali katika huduma hii na utume huu, alioukosa Yuda, aende zake mahali pake mwenyewe. 26 Wakawapigia kura; kura ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na mmoja.

Matendo ya Mitume 2

1 Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. 2 Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. 3 Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. 4 Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka. 5 Na walikuwako Yerusalemu Wayahudi wakikaa, watu watauwa, watu wa kila taifa chini ya mbingu. 6 Basi sauti hii iliposikiwa makutano walikutanika, wakashikwa na fadhaa, kwa kuwa kila mmoja aliwasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe. 7 Wakashangaa wote, wakastaajabu wakiambiana, Tazama, hawa wote wasemao si Wagalilaya? 8 Imekuwaje basi sisi kusikia kila mtu lugha yetu tuliyozaliwa nayo? 9 Warparthi na Wamedi na Waelami, nao wakaao Mesopotamia, Uyahudi na Kapadokia, Ponto na Asia, 10 Frigia na Pamfilia, Misri na pande za Libia karibu na Kirene, na wageni watokao Rumi, Wayahudi na waongofu, 11 Wakrete na Waarabu; tunawasikia hawa wakisema kwa lugha zetu matendo makuu ya Mungu. 12 Wakashangaa wote wakaingiwa na shaka, wakiambiana, Maana yake nini mambo haya? 13 Wengine walidhihaki, wakisema, wamelewa kwa mvinyo mpya. 14 Lakini Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkasikilize maneno yangu. 15 Sivyo mnavyodhani; watu hawa hawakulewa, kwa maana ni saa tatu ya mchana; 16 lakini jambo hili ni lile lililonenwa kwa kinywa cha nabii Yoeli, 17 Itakuwa siku za mwisho, asema Mungu, nitawamwagia watu wote Roho yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto. 18 Naam, na siku zile nitawamwagia watumishi wangu wanaume na wanawake Roho yangu, nao watatabiri. 19 Nami nitatoa ajabu katika mbingu juu, na ishara katika nchi chini, damu na moto, na mvuke wa moshi. 20 Jua litageuka kuwa giza, na mwezi kuwa damu, kabla ya kuja ile siku ya Bwana iliyo kuu na iliyo dhahiri. 21 Na itakuwa kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa. 22 Enyi waume wa Israeli, sikilizeni maneno haya: Yesu wa Nazareti, mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake kati yenu, kama ninyi wenyewe mnavyojua; 23 mtu huyu alipotolewa kwa shauri la Mungu lililokusudiwa, na kwa kujua kwake tangu zamani, ninyi mkamsulibisha kwa mikono ya watu wabaya, mkamwua; 24 ambaye Mungu alimfufua, akiufungua uchungu wa mauti, kwa sababu haikuwezekana ashikwe nao. 25 Maana Daudi ataja habari zake, Nalimwona Bwana mbele yangu siku zote, Kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike. 26 Kwa hiyo moyo wangu ukapendezewa, ulimi wangu ukafurahi; Tena mwili wangu nao utakaa katika matumaini. 27 Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu; Wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu. 28 Umenijuvisha njia za uzima; Utanijaza furaha kwa uso wako. 29 Waume, ndugu zangu, mniwie radhi, niseme kwa ujasiri mbele yenu habari za baba yetu mkuu, Daudi, ya kuwa alifariki akazikwa, na kaburi lake liko kwetu hata leo. 30 Basi kwa kuwa ni nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi; 31 yeye mwenyewe akitangulia kuyaona haya, alitaja habari za kufufuka kwake Kristo, ya kwamba roho yake haikuachwa kuzimu, wala mwili wake haukuona uharibifu. 32 Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake. 33 Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya Roho Mtakatifu, amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia. 34 Maana Daudi hakupanda mbinguni; bali yeye mwenyewe anasema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Keti upande wa mkono wangu wa kuume. 35 Hata nitakapowaweka adui zako chini ya miguu yako. 36 Basi nyumba yote ya Israeli na wajue yakini ya kwamba Mungu amemfanya Yesu huyo mliyemsulibisha kuwa Bwana na Kristo. 37 Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu? 38 Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu. 39 Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie. 40 Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya, akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi. 41 Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu. 42 Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali. 43 Kila mtu akaingiwa na hofu; ajabu nyingi na ishara zikafanywa na mitume. 44 Na wote walioamini walikuwa mahali pamoja, na kuwa na vitu vyote shirika, 45 wakiuza mali zao, na vitu vyao walivyokuwa navyo, na kuwagawia watu wote kama kila mtu alivyokuwa na haja. 46 Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakimega mkate nyumba kwa nyumba, na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe, 47 wakimsifu Mungu, na kuwapendeza watu wote. Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa.

Matendo ya Mitume 3

1 Basi Petro na Yohana walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali, saa tisa. 2 Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu, ambaye walimweka kila siku katika mlango wa hekalu uitwao Mzuri, ili aombe sadaka kwa watu waingiao ndani ya hekalu. 3 Mtu huyu akiwaona Petro na Yohana wakiingia hekaluni aliomba apewe sadaka. 4 Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. 5 Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. 6 Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. 7 Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu. 8 Akaondoka upesi akasimama, akaanza kwenda; akaingia ndani ya hekalu pamoja nao, akienda, akiruka-ruka, na kumsifu Mungu. 9 Watu wote wakamwona akienda, akimsifu Mungu. 10 Wakamtambua, ya kuwa yeye ndiye aliyekuwa akiketi na kuomba sadaka penye mlango Mzuri wa hekalu; wakajaa ushangao wakastaajabia mambo yale yaliyompata. 11 Basi alipokuwa akiwashika Petro na Yohana, watu wote wakawakusanyikia mbio katika tao lile lililoitwa tao la Sulemani, wakishangaa sana. 12 Hata Petro alipoyaona haya akawajibu wale watu, Enyi Waisraeli, mbona mnastaajabia haya, au mbona mnatukazia macho sisi, kana kwamba tumemfanya huyu aende kwa nguvu zetu sisi, au kwa utauwa wetu sisi? 13 Mungu wa Ibrahimu na wa Isaka na wa Yakobo, Mungu wa baba zetu, amemtukuza mtumishi wake Yesu, ambaye ninyi mlimsaliti na kumkana mbele ya Pilato, alipokuwa ametoa hukumu yake afunguliwe. 14 Bali ninyi mlimkana yule Mtakatifu, yule Mwenye haki, mkataka mpewe mwuaji; 15 mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi wake. 16 Na kwa imani katika jina lake, jina lake limemtia nguvu mtu huyu mnayemwona na kumjua; na imani ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele yenu ninyi nyote. 17 Basi sasa, ndugu, najua ya kuwa mliyatenda haya kwa kutokujua kwenu, kama na wakuu wenu walivyotenda. 18 Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo. 19 Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; 20 apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani; 21 ambaye ilimpasa kupokewa mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa ulimwengu. 22 Kwa maana Musa kweli alisema ya kwamba, Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu, kama mimi; msikieni yeye katika mambo yote atakayonena nanyi. 23 Na itakuwa ya kwamba kila mtu asiyemsikiliza nabii huyo ataangamizwa na kutengwa na watu wake. 24 Naam, na manabii wote tangu Samweli na wale waliokuja baada yake, wote walionena, walihubiri habari za siku hizi. 25 Ninyi mmekuwa watoto wa manabii na wa maagano yale, ambayo Mungu aliagana na baba zenu, akimwambia Ibrahimu, Katika uzao wako kabila zote za ulimwengu zitabarikiwa. 26 Mungu, akiisha kumfufua mtumishi wake Yesu, alimtuma kwenu ninyi kwanza, ili kuwabarikia kwa kumwepusha kila mmoja wenu na maovu yake.

Matendo ya Mitume 4

1 Hata walipokuwa wakisema na watu wale, makuhani na akida wa hekalu na Masadukayo wakawatokea, 2 wakifadhaika sana kwa sababu wanawafundisha watu na kuhubiri katika Yesu ufufuo wa wafu. 3 Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa imekwisha kuwa jioni. 4 Lakini wengi katika hao waliosikia lile neno waliamini; na hesabu ya watu waume ikawa kama elfu tano. 5 Hata asubuhi wakubwa na wazee na waandishi wakakusanyika Yerusalemu, 6 na Anasi Kuhani Mkuu, na Kayafa pia, na Yohana na Iskanda, na wote wale waliokuwa jamaa zake Kuhani Mkuu. 7 Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya? 8 Ndipo Petro, akijaa Roho Mtakatifu, akawaambia, Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, 9 kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, 10 jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. 11 Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. 12 Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo. 13 Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu. 14 Na wakimwona yule aliyeponywa akisimama pamoja nao hawakuwa na neno la kujibu. 15 Wakawaamuru kutoka katika baraza, wakafanya shauri wao kwa wao, 16 wakisema, Tuwafanyie nini watu hawa? Maana ni dhahiri kwa watu wote wakaao Yerusalemu ya kwamba ishara mashuhuri imefanywa nao, wala hatuwezi kuikana. 17 Lakini neno hili lisije likaenea katika watu, na tuwatishe wasiseme tena na mtu awaye yote kwa jina hili. 18 Wakawaita, wakawaamuru wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu. 19 Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; 20 maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia. 21 Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka; 22 maana umri wake yule mtu aliyefanyiwa ishara hii ya kuponya ulipita miaka arobaini. 23 Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao, wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. 24 Nao waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; 25 nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili? 26 Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake. 27 Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, 28 ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. 29 Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, 30 ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu. 31 Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri. 32 Na jamii ya watu walioamini walikuwa na moyo mmoja na roho moja; wala hapana mmoja aliyesema ya kuwa kitu cho chote alicho nacho ni mali yake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote shirika. 33 Na mitume wakatoa ushuhuda wa kufufuka kwake Yesu kwa nguvu nyingi, na neema nyingi ikawa juu yao wote. 34 Wala hapakuwa na mtu mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa, 35 wakaiweka miguuni pa mitume; kila mtu akagawiwa kwa kadiri ya alivyohitaji. 36 Na Yusufu, aliyeitwa na mitume Barnaba, (maana yake, Mwana wa faraja), Mlawi, asili yake ni mtu wa Kipro, 37 alikuwa na shamba akaliuza, akaileta fedha, akaiweka miguuni pa mitume.

Matendo ya Mitume 5

1 Lakini mtu mmoja jina lake Anania, pamoja na Safira mkewe, aliuza mali, 2 akazuia kwa siri sehemu ya thamani yake, mkewe naye akijua haya, akaleta fungu moja akaliweka miguuni pa mitume. 3 Petro akasema, Anania, kwa nini Shetani amekujaza moyo wako kumwambia uongo Roho Mtakatifu, na kuzuia kwa siri sehemu ya thamani ya kiwanja? 4 Kilipokuwa kwako, hakikuwa mali yako? Na kilipokuwa kimekwisha kuuzwa, thamani yake haikuwa katika uwezo wako? Ilikuwaje hata ukaweka neno hili moyoni mwako? Hukumwambia uongo mwanadamu, bali Mungu. 5 Anania aliposikia maneno haya akaanguka, akafa. Hofu nyingi ikawapata watu wote walioyasikia haya. 6 Vijana wakaondoka, wakamtia katika sanda, wakamchukua nje, wakamzika. 7 Hata muda wa saa tatu baadaye mkewe akaingia, naye hana habari ya hayo yaliyotokea. 8 Petro akamjibu, Niambie, Mlikiuza kiwanja kwa thamani hiyo? Akasema, Ndiyo, kwa thamani hiyo. 9 Petro akamwambia, Imekuwaje hata mkapatana kumjaribu Roho wa Bwana? Angalia, miguu yao waliomzika mumeo ipo mlangoni, nao watakuchukua nje wewe nawe. 10 Mara akaanguka miguuni pake akafa; wale vijana wakaingia wakamkuta amekufa, wakamchukua nje, wakamzika pamoja na mumewe. 11 Hofu nyingi ikawapata kanisa lote na watu wote walioyasikia haya. 12 Na kwa mikono ya mitume zikafanyika ishara na maajabu mengi katika watu; nao wote walikuwako kwa nia moja katika ukumbi wa Sulemani; 13 na katika wote wengine hapana hata mmoja aliyethubutu kuambatana nao; ila watu waliwaadhimisha; 14 walioamini wakazidi kuongezeka kwa Bwana, wengi, wanaume na wanawake; 15 hata ikawa katika njia kuu hutoa nje wagonjwa, na kuwaweka juu ya majamvi na magodoro, ili Petro akija, ngawa kivuli chake kimwangukie mmojawapo wao. 16 Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa. 17 Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, 18 wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; 19 lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, 20 Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu. 21 Nao waliposikia wakaenda alfajiri hekaluni, wakaanza kufundisha. Akaja Kuhani Mkuu nao waliokuwa pamoja naye, wakawakutanisha watu wa baraza, na wazee wote wa wana wa Israeli, wakatuma watu gerezani ili wawalete. 22 Hata watumishi walipofika hawakuwaona gerezani, wakarudi wakatoa habari, 23 wakisema, Gereza tumeikuta imefungwa salama, nao walinzi wamesimama mbele ya mlango; lakini tulipoufungua hatukukuta mtu ndani. 24 Basi jemadari wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia haya, wakaingiwa na shaka kwa ajili yao, litakuwaje jambo hilo. 25 Mtu mmoja akaja akawapasha habari ya kwamba, Watu wale mliowaweka gerezani wako ndani ya hekalu, wamesimama wakiwafundisha watu. 26 Ndipo yule jemadari akaenda pamoja na watumishi, wakawaleta, lakini si kwa nguvu, kwa maana waliogopa watu wasije wakawapiga kwa mawe. 27 Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, 28 akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. 29 Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. 30 Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. 31 Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi. 32 Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na Roho Mtakatifu ambaye Mungu amewapa wote wamtiio. 33 Wao waliposikia wakachomwa mioyo yao; wakafanya shauri kuwaua. 34 Lakini mtu mmoja, Farisayo, jina lake Gamalieli, mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa na watu wote, akasimama katika baraza, akaamuru mitume wawekwe nje kitambo kidogo, 35 akawaambia, Enyi waume wa Israeli, jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu hawa. 36 Kwa sababu kabla ya siku hizi aliondoka Theuda, akijidai ya kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu. 37 Baada ya mtu huyo aliondoka Yuda Mgalilaya, siku zile za kuandikiwa orodha, akawavuta watu kadha wa kadha nyuma yake, naye pia akapotea na wote waliomsadiki wakatawanyika. 38 Basi sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, 39 lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu. 40 Wakakubali maneno yake; nao walipowaita mitume, wakawapiga, wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao. 41 Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo. 42 Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.

Matendo ya Mitume 6

1 Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. 2 Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. 3 Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; 4 na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno. 5 Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; 6 ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao. 7 Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani. 8 Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. 9 Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; 10 lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. 11 Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. 12 Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. 13 Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; 14 maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa. 15 Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika.

Matendo ya Mitume 7

1 Kuhani Mkuu akasema, Je! Mambo hayo ndivyo yalivyo? 2 Naye akasema, Ndugu zangu na baba zangu, sikilizeni: Mungu wa utukufu alimtokea baba yetu Ibrahimu, alipokuwa katika Mesopotamia, kabla hajakaa Harani, 3 akamwambia, Toka katika nchi yako na katika jamaa zako, ukaende hata nchi nitakayokuonyesha. 4 Ndipo alipotoka katika nchi ya Wakaldayo, akakaa Harani, akatoka huko baada ya kufa babaye, Mungu akamhamisha mpaka nchi hii mnayokaa ninyi sasa. 5 Wala hakumpa urithi humu hata kiasi cha kuweka mguu; akaahidi kwamba atampa, iwe milki yake, na ya uzao wake baadaye alipokuwa hana mtoto. 6 Mungu akanena hivi, ya kwamba wazao wake watakuwa wageni katika nchi ya watu wengine, nao watawafanya kuwa watumwa wao, na kuwatenda mabaya kwa muda wa miaka mia nne. 7 Na lile taifa watakaowafanya watumwa nitawahukumu mimi, alisema Mungu; na baada ya hayo watatoka, nao wataniabudu mahali hapa. 8 Akampa agano la tohara; basi Ibrahimu akamzaa Isaka, akamtahiri siku ya nane. Isaka akamzaa Yakobo. Yakobo akawazaa wale kumi na wawili, wazee wetu. 9 Wale wazee wetu wakimwonea wivu Yusufu, wakamwuza aende Misri. Mungu akawa pamoja naye, 10 akamtoa katika dhiki zake zote, akampa fadhili na hekima mbele ya Farao, mfalme wa Misri; naye akamfanya awe mtawala juu ya Misri na nyumba yake yote. 11 Basi kukawa njaa katika nchi yote ya Misri na Kanaani, na dhiki nyingi, wala baba zetu hawakupata chakula cha kuwatosha. 12 Hata Yakobo aliposikia ya kwamba huko Misri kuna nafaka, akawatuma baba zetu mara ya kwanza. 13 Hata safari ya pili Yusufu akajitambulisha kwa ndugu zake, jamaa ya Yusufu ikawa dhahiri kwa Farao. 14 Yusufu akatuma watu akamwita Yakobo babaye na jamaa zake wote pia, watu sabini na watano. 15 Basi Yakobo akashuka mpaka Misri; akafa yeye na baba zetu; 16 wakachukuliwa mpaka Shekemu wakazikwa katika kaburi lile, ambalo Ibrahimu alilinunua kwa kima cha fedha kwa wana wa Hamori, huko Shekemu. 17 Basi wakati wa ile ahadi ambayo Mungu alimpa Ibrahimu ulipokuwa unakaribia, wale watu wakazidi na kuongezeka sana huko Misri, 18 hata mfalme mwingine akainuka juu ya Misri, asiyemfahamu Yusufu. 19 Huyo akawafanyia hila kabila yetu, na kuwatenda mabaya baba zetu, akiwaamuru wawatupe watoto wao wachanga, ili wasiishi. 20 Wakati huo akazaliwa Musa, naye alikuwa mzuri sana, akalelewa muda wa miezi mitatu katika nyumba ya babaye. 21 Hata alipotupwa, binti Farao akamtwaa, akamlea awe kama mwanawe. 22 Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri, akawa hodari wa maneno na matendo. 23 Umri wake ulipopata kama miaka arobaini akaazimu moyoni mwake kwenda kuwatazama ndugu zake Waisraeli. 24 Akamwona mmoja akidhulumiwa, akamtetea, akamlipia kisasi yule aliyekuwa akionewa, akampiga huyo Mmisri. 25 Alidhani kwamba ndugu zake watafahamu ya kuwa Mungu anawapa wokovu kwa mkono wake, lakini hawakufahamu. 26 Siku ya pili yake akawatokea walipokuwa wakishindana, akataka kuwapatanisha, akisema, Enyi bwana zangu, ninyi ni ndugu. Mbona mnadhulumiana? 27 Lakini yeye aliyemdhulumu mwenziwe akamsukumia mbali, akisema, Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mkuu na mwamuzi juu yetu? 28 Je! Wataka kuniua mimi kama ulivyomwua yule Mmisri jana? 29 Musa akakimbia kwa neno hilo, akakaa hali ya ugeni katika nchi ya Midiani, akazaa wana wawili huko. 30 Hata miaka arobaini ilipotimia, malaika wa Bwana akamtokea katika jangwa la mlima wa Sinai katika mwali wa moto, kijitini. 31 Musa alipouona, akastaajabia maono yale, na alipokaribia ili atazame, sauti ya Bwana ikamjia, 32 Mimi ni Mungu wa baba zako, Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akatetemeka, asithubutu kutazama. 33 Bwana akamwambia, Vua viatu miguuni mwako, kwa maana mahali hapa unaposimama ni nchi takatifu. 34 Yakini nimeona mateso ya watu wangu waliomo Misri, nimesikia kuugua kwao, nami nimeshuka niwatoe. Basi sasa, nitakutuma mpaka Misri. 35 Musa huyo waliyemkataa, wakisema, Ni nani aliyekuweka kuwa mkuu na mwamuzi? Ndiye aliyetumwa na Mungu kuwa mkuu na mkombozi, kwa mkono wa yule malaika aliyemtokea katika kile kijiti. 36 Huyo ndiye aliyewatoa, akifanya ajabu na ishara katika nchi ya Misri, na katika bahari ya Shamu, na katika jangwa muda wa miaka arobaini. 37 Musa huyo ndiye aliyewaambia Waisraeli, Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu, kama mimi; msikieni yeye. 38 Yeye ndiye aliyekuwa katika kanisa jangwani pamoja na yule malaika aliyesema naye katika mlima wa Sinai, tena pamoja na baba zetu; ndiye aliyepokea maneno ya uzima atupe sisi. 39 Mtu huyo baba zetu hawakutaka kumtii, bali wakamsukumia mbali, na kwa mioyo yao wakarejea Misri, 40 wakamwambia Haruni, Tufanyie miungu, watakaotutangulia; maana huyo Musa, aliyetutoa katika nchi ya Misri, hatujui lililompata. 41 Wakafanya ndama siku zile, wakaleta dhabihu kwa sanamu ile, wakafurahia kazi za mikono yao. 42 Basi Mungu akaghairi, akawaacha ili waliabudu jeshi la mbinguni, kama ilivyoandikwa katika chuo cha manabii, Je! Mlinitolea mimi dhabihu na sadaka Miaka arobaini katika jangwa, enyi nyumba ya Israeli? 43 Nanyi mlichukua hema ya Moleki, Na nyota za mungu wenu Refani, Sanamu mlizozifanya ili kuziabudu; Nami nitawafahamisha mwende mbali kupita Babeli. 44 Ile hema ya ushahidi ilikuwa pamoja na baba zetu jangwani, kama alivyoagiza yeye aliyesema na Musa, ya kwamba aifanye sawasawa na mfano ule aliouona; 45 ambayo baba zetu, kwa kupokezana, wakaiingiza pamoja na Yoshua katika milki ya Mataifa wale, ambao Mungu aliwafukuza mbele ya baba zetu, mpaka siku za Daudi; 46 aliyepata fadhili mbele za Mungu, naye aliomba ampatie Mungu wa Yakobo maskani. 47 Lakini Sulemani alimjengea nyumba. 48 Ila Yeye aliye juu hakai katika nyumba zilizofanywa kwa mikono, kama vile asemavyo nabii, 49 Mbingu ni kiti changu cha enzi, Na nchi ni pa kuwekea miguu yangu; Ni nyumba gani mtakayonijengea? Asema Bwana, 50 Au ni mahali gani nitakapostarehe? Si mkono wangu uliofanya haya yote? 51 Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, siku zote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo. 52 Ni yupi katika manabii ambaye baba zenu hawakumwudhi? Nao waliwaua wale waliotabiri habari za kuja kwake yule Mwenye Haki; ambaye ninyi sasa mmekuwa wasaliti wake, mkamwua; 53 ninyi mlioipokea torati kwa agizo la malaika msiishike. 54 Basi waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno. 55 Lakini yeye akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu. 56 Akasema, Tazama! Naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu. 57 Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, 58 wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. 59 Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu. 60 Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.

Matendo ya Mitume 8

1 Siku ile kukatukia adha kuu ya kanisa lililokuwa katika Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao mitume. 2 Watu watauwa wakamzika Stefano, wakamfanyia maombolezo makuu. 3 Sauli akaliharibu kanisa, akiingia kila nyumba, na kuwaburuta wanaume na wanawake na kuwatupa gerezani. 4 Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno. 5 Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, akawahubiri Kristo. 6 Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. 7 Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. 8 Ikawa furaha kubwa katika mji ule. 9 Na mtu mmoja, jina lake Simoni, hapo kwanza alikuwa akifanya uchawi katika mji ule, akiwashangaza watu wa taifa la Wasamaria, akisema ya kuwa yeye ni mtu mkubwa. 10 Wote wakamsikiliza tangu mdogo hata mkubwa, wakisema, Mtu huyu ni uweza wa Mungu, ule Mkuu. 11 Wakamsikiliza, kwa maana amewashangaza muda mwingi kwa uchawi wake. 12 Lakini walipomwamini Filipo, akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu, na jina lake Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na wanawake. 13 Na yeye Simoni mwenyewe aliamini akabatizwa, akashikamana na Filipo; akashangaa alipoziona ishara na miujiza mikubwa inayotendeka. 14 Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana; 15 ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu; 16 kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu. 17 Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. 18 Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema, 19 Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu, apokee Roho Mtakatifu. 20 Lakini Petro akamwambia, Fedha yako na ipotelee mbali pamoja nawe, kwa kuwa umedhania ya kuwa karama ya Mungu yapatikana kwa mali. 21 Huna fungu wala huna sehemu katika jambo hili, kwa kuwa moyo wako si mnyofu mbele za Mungu. 22 Basi, tubia uovu wako huu, ukamwombe Bwana, ili kama yamkini, usamehewe fikira hii ya moyo wako. 23 Kwa maana nakuona u katika uchungu kama nyongo, na tena u katika kifungo cha uovu. 24 Simoni akajibu, akasema, Niombeeni ninyi kwa Bwana, yasinifikilie mambo haya mliyosema hata moja. 25 Nao walipokwisha kushuhudia na kulihubiri neno la Bwana wakarudi Yerusalemu, wakaihubiri Injili katika vijiji vingi vya Wasamaria. 26 Malaika wa Bwana akasema na Filipo, akamwambia, Ondoka ukaende upande wa kusini hata njia ile itelemkayo kutoka Yerusalemu kwenda Gaza; nayo ni jangwa. 27 Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu, 28 akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. 29 Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo. 30 Basi Filipo akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! Yamekuelea haya unayosoma? 31 Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza? Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. 32 Na fungu la Maandiko alilokuwa akilisoma ni hili, Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, Na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, Vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. 33 Katika kujidhili kwake hukumu yake iliondolewa. Ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi. 34 Yule towashi akamjibu Filipo, akasema, Nakuomba, nabii huyu; asema maneno haya kwa habari ya nani; ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine? 35 Filipo akafunua kinywa chake, naye, akianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu. 36 Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; yule towashi akasema, Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe? 37 Filipo akasema, Ukiamini kwa moyo wako wote, inawezekana. Akajibu, akanena, Naamini ya kwamba Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu. 38 Akaamuru lile gari lisimame; wakatelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi; naye akambatiza. 39 Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda zake akifurahi. 40 Lakini Filipo akaonekana katika Azoto, na alipokuwa akipita akahubiri Injili katika miji yote, hata akafika Kaisaria.

Matendo ya Mitume 9

1 Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu, 2 akataka ampe barua za kuenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu. 3 Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. 4 Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? 5 Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. 6 Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda. 7 Na wale watu waliosafiri pamoja naye wakasimama kimya, wakiisikia sauti, wasione mtu. 8 Sauli akainuka katika nchi, na macho yake yalipofumbuka, hakuona kitu; wakamshika mkono wakamleta mpaka Dameski. 9 Akawa siku tatu haoni; hali, wala hanywi. 10 Basi palikuwapo Dameski mwanafunzi jina lake Anania. Bwana akamwambia katika maono, Anania. Akasema, Mimi hapa, Bwana. 11 Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana, angalia, anaomba; 12 naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea mikono juu yake, apate kuona tena. 13 Lakini Anania akajibu, Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; 14 hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako. 15 Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli. 16 Maana nitamwonyesha yalivyo mengi yatakayompasa kuteswa kwa ajili ya Jina langu. 17 Anania akaenda zake, akaingia mle nyumbani; akamwekea mikono akisema, Ndugu Sauli, Bwana amenituma, Yesu, yeye aliyekutokea katika njia uliyoijia, upate kuona tena, ukajazwe Roho Mtakatifu. 18 Mara vikaanguka machoni pake vitu kama magamba, akapata kuona, akasimama, akabatizwa; 19 akala chakula, na kupata nguvu. Akawa huko siku kadha wa kadha pamoja na wanafunzi walioko Dameski. 20 Mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. 21 Na wote waliosikia wakashangaa, wakasema, Siye huyu aliyewaharibu walioliitia Jina hili huko Yerusalemu? Na hapa alikuwa amekuja kwa kusudi hilo, awafunge na kuwapeleka kwa wakuu wa makuhani? 22 Sauli akazidi kuwa hodari, akawatia fadhaa Wayahudi waliokaa Dameski, akithibitisha ya kuwa huyu ndiye Kristo. 23 Hata siku nyingi zilipopita, Wayahudi wakafanya shauri ili wamwue; 24 lakini hila yao ikajulikana na Sauli. Wakamvizia malangoni mchana na usiku wapate kumwua. 25 Wanafunzi wake wakamtwaa usiku wakamshusha ukutani, wakimtelemsha katika kapu. 26 Na Sauli alipofika Yerusalemu, alijaribu kujiunga na wanafunzi, nao walikuwa wakimwogopa wote, wasisadiki ya kuwa yeye ni mwanafunzi. 27 Lakini Barnaba akamtwaa, akampeleka kwa mitume, akawaeleza jinsi alivyomwona Bwana njiani, na ya kwamba alisema naye, na jinsi alivyohubiri kwa ushujaa katika Dameski kwa jina la Yesu. 28 Naye akawa pamoja nao katika Yerusalemu akiingia na kutoka. 29 Akahubiri kwa jina la Bwana kwa ushujaa, akinena na kuhojiana na Wayahudi wa Kiyunani. Nao wakajaribu kumwua. 30 Lakini ndugu walipopata habari wakamchukua mpaka Kaisaria, wakampeleka aende Tarso. 31 Basi kanisa likapata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu. 32 Hata Petro alipokuwa akizunguka-zunguka pande zote akawatelemkia na watakatifu waliokaa Lida. 33 Akamwona mtu mmoja huko, jina lake Ainea, mtu huyo amelala kitandani miaka minane; maana alikuwa amepooza. 34 Petro akamwambia, Ainea, Yesu Kristo akuponya; ondoka, ujitandikie. Mara akaondoka. 35 Na watu wote waliokaa Lida na Sharoni wakamwona, wakamgeukia Bwana. 36 Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. 37 Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. 38 Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu. 39 Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao. 40 Petro akawatoa nje wote, akapiga magoti, akaomba, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. 41 Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai. 42 Ikajulikana katika mji mzima wa Yafa; watu wengi wakamwamini Bwana. 43 Basi Petro akakaa siku kadha wa kadha huko Yafa, nyumbani mwa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi.

Matendo ya Mitume 10

1 Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, 2 mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima. 3 Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! 4 Akamtazama sana, akaogopa akasema, Kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na sadaka zako zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. 5 Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. 6 Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani, atakuambia yakupasayo kutenda. 7 Na yule malaika aliyesema naye akiisha kuondoka, Kornelio akawaita wawili katika watumishi wake wa nyumbani, na askari mmoja, mtu mtauwa katika wale waliomhudumia daima; 8 na alipokwisha kuwaeleza mambo yote akawatuma kwenda Yafa. 9 Hata siku ya pili, walipokuwa wakisafiri na kuukaribia mji, Petro alipanda juu darini, kwenda kuomba, yapata saa sita ya mchana; 10 akaumwa na njaa sana, akataka kula; lakini walipokuwa wakiandaa, roho yake ikazimia, 11 akaona mbingu zimefunuka, na chombo kikishuka kama nguo kubwa, inatelemshwa kwa pembe zake nne hata nchi; 12 ambayo ndani yake walikuwamo aina zote za wanyama wenye miguu minne, na hao watambaao, na ndege wa angani. 13 Kisha sauti ikamjia, kusema, Ondoka, Petro, uchinje ule. 14 Lakini Petro akasema, Hasha, Bwana, kwa maana sijakula kamwe kitu kilicho kichafu au najisi. 15 Sauti ikamjia mara ya pili, ikimwambia, Vilivyotakaswa na Mungu, usiviite wewe najisi. 16 Jambo hili likatendeka mara tatu; kisha kile chombo kikapokewa tena mbinguni. 17 Hata Petro alipokuwa akiona shaka ndani ya nafsi yake, maana yake ni nini maono hayo aliyoyaona, wale watu waliotumwa na Kornelio, wakiisha kuiulizia nyumba ya Simoni, wakasimama mbele ya mlango, 18 wakaita; wakauliza kwamba Simoni aitwaye Petro anakaa humo. 19 Na Petro alikuwa akiyafikiri yale maono. Roho akamwambia, Wako watu watatu wanakutafuta. 20 Basi ondoka ushuke ufuatane nao, usione tashwishi, kwa maana ni mimi niliyewatuma. 21 Petro akawashukia wale watu, akanena, Mimi ndiye mnayemtafuta. Mmekuja kwa sababu gani? 22 Wakasema, Kornelio akida, mtu mwenye haki, mchaji wa Mungu, aliye na sifa njema kwa taifa lote la Wayahudi, alionywa na malaika mtakatifu kutuma watu kwako, uende nyumbani kwake, apate kusikiliza maneno kwako. 23 Akawakaribisha wawe wageni wake. Hata siku ya pili, Petro akaondoka akatoka pamoja nao, na baadhi ya ndugu waliokaa Yafa wakafuatana naye. 24 Siku ya pili yake wakaingia Kaisaria. Na Kornelio alikuwa akiwangojea, hali amekusanya jamaa zake na rafiki zake. 25 Petro alipokuwa akiingia Kornelio akatoka amlaki akamwangukia miguu, akamsujudia. 26 Lakini Petro akamwinua, akasema, Simama, mimi nami ni mwanadamu. 27 Na katika kusema naye akaingia ndani, akaona watu wengi wamekusanyika. 28 Akawaambia, Ninyi mnajua ya kuwa si halali mtu aliye Myahudi ashikamane na mtu aliye wa taifa lingine wala kumwendea, lakini Mungu amenionya, nisimwite mtu awaye yote mchafu wala najisi. 29 Kwa sababu hiyo nalikuja nilipoitwa, nisikatae; basi nawauliza, ni neno gani mliloniitia? 30 Kornelio akasema, Siku tatu zilizopita, katika saa ii hii, yaani saa tisa, nilikuwa nikisali nyumbani mwangu; nikamwona mtu amesimama mbele yangu, mwenye nguo zing'arazo, 31 akasema, Kornelio, kuomba kwako kumesikiwa, na sadaka zako zinakumbukwa mbele za Mungu. 32 Basi, tuma watu kwenda Yafa, ukamwite Simoni aitwaye Petro, anakaa katika nyumba ya Simoni, mtengenezaji wa ngozi, karibu na pwani; naye akija atasema nawe. 33 Mara nikatuma watu kwako, nawe umefanya vyema kuja. Basi sasa sisi sote tupo hapa mbele za Mungu, tupate kuyasikiliza maneno yote uliyoamriwa na Bwana. 34 Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; 35 bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye. 36 Neno lile alilowapelekea wana wa Israeli akihubiri habari njema ya amani kwa Yesu Kristo (ndiye Bwana wa wote), 37 jambo lile ninyi mmelijua, lililoenea katika Uyahudi wote likianzia Galilaya, baada ya ubatizo aliouhubiri Yohana; 38 habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye. 39 Nasi tu mashahidi wa mambo yote aliyoyatenda katika nchi ya Wayahudi na katika Yerusalemu; ambaye walimwua wakamtundika mtini. 40 Huyo Mungu alimfufua siku ya tatu, akamjalia kudhihirika, 41 si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliokuwa wamekwisha kuchaguliwa na Mungu, ndio sisi, tuliokula na kunywa pamoja naye baada ya kufufuka kwake kutoka kwa wafu. 42 Akatuagiza tuwahubiri watu na kushuhudia ya kuwa huyu ndiye aliyeamriwa na Mungu awe Mhukumu wa walio hai na wafu. 43 Huyo manabii wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la dhambi. 44 Petro alipokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashukia wote waliolisikia lile neno. 45 Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. 46 Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu, 47 Ni nani awezaye kuzuia maji, hawa wasibatizwe, watu waliopokea Roho Mtakatifu vile vile kama sisi? 48 Akaamuru wabatizwe kwa Jina lake Yesu Kristo. Ndipo wakamsihi azidi kukaa siku kadha wa kadha.

Matendo ya Mitume 11

1 Basi mitume na ndugu waliokuwako katika Uyahudi wakapata habari ya kwamba watu wa Mataifa nao wamelipokea neno la Mungu. 2 Na Petro alipopanda kwenda Yerusalemu, wale walio wa tohara wakashindana naye, 3 wakisema, Uliingia kwa watu wasiotahiriwa ukala nao. 4 Petro akaanza kuwaeleza kwa taratibu, akasema, 5 Nalikuwa katika mji wa Yafa, nikiomba, roho yangu ikazimia, nikaona maono; chombo kinashuka, kama nguo kubwa inatelemshwa kutoka mbinguni kwa pembe zake nne, kikanifikilia. 6 Nikakitazama sana, nikifikiri, nikaona wanyama wa nchi wenye miguu minne, na wanyama wa mwituni, nao watambaao, na ndege wa angani. 7 Nikasikia na sauti ikiniambia, Ondoka, Petro, ukachinje ule. 8 Nikasema, Hasha, Bwana, kwa maana kitu kilicho kichafu au kilicho najisi hakijaingia kabisa kinywani mwangu. 9 Sauti ikanijibu mara ya pili kutoka mbinguni, Alivyovitakasa Mungu, usivinene wewe najisi. 10 Jambo hili likatendeka mara tatu, kisha vitu vyote vikavutwa tena juu mbinguni. 11 Na tazama, mara hiyo watu watatu wakasimama mbele ya nyumba tuliyokuwamo, waliotumwa kwangu kutoka Kaisaria. 12 Roho akaniambia nifuatane nao, nisione tashwishi. Ndugu hawa sita nao wakaenda pamoja nami, tukaingia katika nyumba ya mtu yule; 13 akatueleza jinsi alivyomwona malaika aliyesimama nyumbani mwake na kumwambia, Tuma watu kwenda Yafa ukamwite Simoni aitwaye Petro, 14 atakayekuambia maneno ambayo yatakuokoa, wewe na nyumba yako yote. 15 Ikawa nilipoanza kunena, Roho Mtakatifu akawashukia kama alivyotushukia sisi mwanzo. 16 Nikalikumbuka neno lile la Bwana, jinsi alivyosema, Yohana alibatiza kwa maji kweli, bali ninyi mtabatizwa kwa Roho Mtakatifu. 17 Basi ikiwa Mwenyezi Mungu amewapa wao karama ile ile aliyotupa sisi tuliomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani niweze kumpinga Mungu? 18 Waliposikia maneno haya wakanyamaza, wakamtukuza Mungu, wakisema, Basi, Mungu amewajalia hata mataifa nao toba liletalo uzima. 19 Basi wale waliotawanyika kwa sababu ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano, wakasafiri hata Foinike na Kipro na Antiokia, wasilihubiri lile neno ila kwa Wayahudi peke yao. 20 Lakini baadhi ya hao walikuwa watu wa Kipro na Kirene, nao walipofika Antiokia wakasema na Wayahudi wa Kiyunani, wakihubiri habari njema za Bwana Yesu. 21 Mkono wa Bwana ukawa pamoja nao, watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana. 22 Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia. 23 Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote waambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. 24 Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana. 25 Kisha akatoka akaenda Tarso kumtafuta Sauli; 26 hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia. 27 Siku zizo hizo manabii walitelemka kutoka Yerusalemu hata Antiokia. 28 Na tulipokusanyika akasimama mmoja wao, jina lake Agabo, akaonyesha kwa uweza wa Roho Mtakatifu kwamba njaa kubwa itakuja karibu katika dunia nzima, nayo ikatukia katika siku za Klaudio. 29 Na wale wanafunzi, kila mtu kwa kadiri ya alivyofanikiwa, wakaazimu kupeleka msaada kwa ndugu zao waliokaa Uyahudi. 30 Wakafanya hivyo, wakawapelekea wazee kwa mikono ya Barnaba na Sauli.

Matendo ya Mitume 12

1 Panapo majira yale yale Herode mfalme akanyosha mikono yake kuwatenda mabaya baadhi ya watu wa kanisa. 2 Akamwua Yakobo, ndugu yake Yohana, kwa upanga. 3 Na akiona ya kuwa imewapendeza Wayahudi akaendelea akamshika na Petro. Siku hizo zilikuwa siku za mikate isiyochachwa. 4 Alipokwisha kumkamata, akamweka gerezani akamtia mikononi mwa vikosi vinne vya askari wanne wanne, wamlinde, akitaka baada ya Pasaka kumtoa na kumweka mbele ya watu. 5 Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili yake. 6 Hata wakati Herode alipotaka kumtoa, usiku ule ule Petro alikuwa analala katikati ya askari wawili, amefungwa minyororo miwili; walinzi mbele ya mlango wakailinda gereza. 7 Mara malaika wa Bwana akasimama karibu naye, nuru ikamulika mle chumbani, akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, Ondoka upesi. Minyororo yake ikamwanguka mikononi. 8 Malaika akamwambia, Jifunge, kavae viatu vyako. Akafanya hivyo. Kisha akamwambia, Jivike nguo yako, ukanifuate. 9 Akatoka nje, akamfuata; wala hakujua ya kuwa ni kweli yaliyofanywa na malaika; bali alidhani kwamba anaona maono. 10 Na walipopita lindo la kwanza na la pili, wakaja hata mlango wa chuma wa kuingilia mjini, ukawafungukia wenyewe. Wakatoka nje, wakapita katika njia moja; mara malaika akamwacha. 11 Hata Petro alipopata fahamu akasema, Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka malaika wake na kunitoa katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa taifa la Wayahudi. 12 Na alipokuwa akifikiri haya akafika nyumbani kwa Mariamu, mamaye Yohana, ambaye jina lake la pili ni Marko; na watu wengi walikuwa wamekutana humo wakiomba. 13 Naye alipobisha kilango cha lango, kijakazi, jina lake Roda, akaja kusikiliza. 14 Alipoitambua sauti ya Petro, hakukifungua lango, kwa ajili ya furaha, bali alipiga mbio, akaingia ndani akawaambia kwamba Petro anasimama mbele ya lango. 15 Wakamwambia, Una wazimu. Lakini yeye akakaza sana, akasema ya kwamba ndivyo hivyo. Wakanena, Ni malaika wake. 16 Petro akafuliza kugonga, hata walipokwisha kumfungulia wakamwona, wakastaajabu. 17 Naye akawapungia mkono wanyamaze, akawaeleza jinsi Bwana alivyomtoa katika gereza. Akasema, Kampasheni Yakobo na wale ndugu habari hizi. Akaondoka, akaenda mahali pengine. 18 Hata kulipopambauka askari wakaingiwa na fadhaa nyingi, amekuwaje Petro. 19 Na Herode alipomtafuta, asimwone, aliwauliza-uliza wale walinzi, akaamuru wauawe. Kisha akatelemkia kutoka Uyahudi kwenda Kaisaria, akakaa huko. 20 Naye Herode alikuwa amewakasirikia sana watu wa Tiro na Sidoni; wakamwendea kwa nia moja, na wakiisha kufanya urafiki na Blasto, mwenye kukitunza chumba cha mfalme cha kulalia, wakataka amani; kwa maana nchi yao ilipata riziki kwa nchi ya mfalme. 21 Basi siku moja iliyoazimiwa, Herode akajivika mavazi ya kifalme, akaketi katika kiti cha enzi, akatoa hotuba mbele yao. 22 Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu. 23 Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho. 24 Neno la Bwana likazidi na kuenea. 25 Na Barnaba na Sauli, walipokwisha kutimiza huduma yao, wakarejea kutoka Yerusalemu, wakamchukua pamoja nao Yohana aitwaye Marko.

Matendo ya Mitume 13

1 Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. 2 Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. 3 Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao. 4 Basi watu hao, wakiisha kupelekwa na Roho Mtakatifu wakatelemkia Seleukia, na kutoka huko wakasafiri baharini hata Kipro. 5 Na walipokuwa katika Salami wakalihubiri neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi, nao walikuwa naye Yohana kuwa mtumishi wao. 6 Walipokwisha kupita katikati ya kisiwa chote mpaka Pafo, wakaona mtu mmoja, mchawi, nabii wa uongo, Myahudi jina lake Bar-Yesu; 7 mtu huyu alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mtu mwenye akili. Yeye liwali akawaita Barnaba na Sauli waje kwake, akataka kulisikia neno la Mungu. 8 Lakini Elima, yule mchawi (maana ndiyo tafsiri ya jina lake), akashindana nao, akitaka kumtia yule liwali moyo wa kuiacha ile imani. 9 Lakini Sauli, ambaye ndiye Paulo, akijaa Roho Mtakatifu, akamkazia macho, 10 akasema, Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za Bwana zilizonyoka? 11 Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda. Mara kiwi kikamwangukia na giza, akazunguka-zunguka na kumtafuta mtu wa kumshika mkono na kumwongoza. 12 Ndipo yule liwali, alipoyaona yaliyotendeka, akaamini, akiyastaajabia mafundisho ya Bwana. 13 Kisha Paulo na wenziwe wakang'oa nanga wakasafiri kutoka Pafo, wakafika Perge katika Pamfilia. Yohana akawaacha akarejea Yerusalemu. 14 Lakini wao wakatoka Perge, wakapita kati ya nchi, wakafika Antiokia, mji wa Pisidia, wakaingia katika sinagogi siku ya sabato, wakaketi. 15 Kisha, baada ya kusomwa torati na chuo cha manabii, wakuu wa sinagogi wakatuma mtu kwao, na kuwaambia, Ndugu, kama mkiwa na neno la kuwafaa watu hawa, lisemeni. 16 Paulo akasimama, akawapungia mkono, akasema, Enyi waume wa Israeli, nanyi mnaomcha Mungu, sikilizeni. 17 Mungu wa watu hawa Israeli aliwachagua baba zetu, akawatukuza watu hao, walipokuwa wakikaa kama wageni katika nchi ya Misri, na kwa mkono ulioinuliwa akawatoa, akawaongoza. 18 Na kwa muda wa miaka kama arobaini akawavumilia katika jangwa. 19 Na alipokwisha kuwaharibu mataifa saba katika nchi ya Kanaani akawapa nchi yao iwe urithi kwa muda wa miaka kama mia nne na hamsini; 20 baada ya hayo akawapa waamuzi hata zamani za nabii Samweli. 21 Hatimaye wakaomba kupewa mfalme; Mungu akawapa Sauli mwana wa Kishi, mtu wa kabila ya Benyamini, kwa muda wa miaka arobaini. 22 Na alipokwisha kumwondoa huyo, akamwinua Daudi awe mfalme wao ambaye alimshuhudia, akisema, Nimemwona Daudi, mwana wa Yese, mtu anayeupendeza moyo wangu, atakayefanya mapenzi yangu yote. 23 Katika uzao wake mtu huyo Mungu amewaletea Israeli Mwokozi, yaani, Yesu, kama alivyoahidi; 24 Yohana alipokuwa amekwisha kuwahubiri watu wote wa Israeli habari za ubatizo wa toba, kabla ya kuja kwake. 25 Naye Yohana alipokuwa akimaliza mwendo wake alinena, Mwanidhani mimi kuwa nani? Mimi siye. Lakini, angalieni, anakuja mmoja nyuma yangu ambaye mimi sistahili kumlegezea viatu vya miguu yake. 26 Ndugu zangu, wana wa ukoo wa Ibrahimu, na hao miongoni mwenu wanaomcha Mungu, kwetu sisi neno la wokovu huu limepelekwa. 27 Kwa maana wakaao Yerusalemu, na wakuu wao, kwa kuwa hawakumjua yeye, wala maneno ya manabii yanayosomwa kila sabato, wameyatimiza kwa kumhukumu. 28 Na ijapokuwa hawakuona sababu ya kumfisha wakamwomba Pilato auawe. 29 Hata walipokwisha kumaliza yote aliyoandikiwa, wakamtelemsha katika ule mti, wakamweka kaburini. 30 Lakini Mungu akamfufua katika wafu; 31 akaonekana siku nyingi na wale waliopanda naye kutoka Galilaya hata Yerusalemu, ambao sasa ndio walio mashahidi wake mbele ya watu. 32 Na sisi tunawahubiri habari njema ya ahadi ile waliyopewa mababa, 33 ya kwamba Mungu amewatimizia watoto wetu ahadi hiyo, kwa kumfufua Yesu; kama ilivyoandikwa katika Zaburi ya pili, Wewe ndiwe Mwanangu, mimi leo nimekuzaa. 34 Tena ya kuwa alimfufua katika wafu, asipate kurudia uharibifu, amenena hivi, Nitawapa ninyi mambo matakatifu ya Daudi yaliyo amini. 35 Kwa hiyo anena na pengine, Hutamwachia Mtakatifu wako kuona uharibifu, 36 Kwa maana Daudi, akiisha kulitumikia shauri la Mungu katika kizazi chake, alilala, akawekwa pamoja na baba zake, akaona uharibifu. 37 Bali huyu aliyefufuliwa na Mungu hakuona uharibifu. 38 Basi, na ijulikane kwenu, ndugu zangu, ya kuwa kwa huyo mnahubiriwa msamaha wa dhambi; 39 na kwa yeye kila amwaminiye huhesabiwa haki katika mambo yale yote asiyoweza kuhesabiwa haki kwa torati ya Musa. 40 Angalieni, basi, isiwajilie habari ile iliyonenwa katika manabii. 41 Tazameni, enyi mnaodharau, kastaajabuni, mkatoweke; kwa kuwa natenda kazi mimi siku zenu, kazi ambayo msingeisadiki kabisa, ijapo mtu akiwasimulia sana. 42 Na walipokuwa wakitoka, wakawasihi waambiwe maneno haya sabato ya pili. 43 Sinagogi ilipofumukana, Wayahudi na waongofu watauwa wengi wakashikamana na Paulo na Barnaba; ambao, wakisema nao, wakawatia moyo kudumu katika neema ya Mungu. 44 Hata sabato ya pili, watu wengi, karibu mji wote, wakakusanyika walisikie neno la Mungu. 45 Bali Wayahudi, walipowaona makutano, wakajaa wivu, wakayakanusha maneno yaliyonenwa na Paulo, wakibisha na kutukana. 46 Paulo na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe kwenu kwanza; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili uzima wa milele, angalieni, twawageukia Mataifa. 47 Kwa sababu ndivyo tulivyoamriwa na Bwana, Nimekuweka uwe nuru ya Mataifa, Upate kuwa wokovu hata mwisho wa dunia. 48 Mataifa waliposikia hayo wakafurahi, wakalitukuza neno la Bwana, nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele wakaamini. 49 Neno la Bwana likaenea katika nchi ile yote. 50 Lakini Wayahudi wakawafitinisha wanawake watauwa wenye cheo na wakuu wa mji, wakawataharakisha watu wawaudhi Paulo na Barnaba; wakawatoa katika mipaka yao. 51 Nao wakawakung'utia mavumbi ya miguu yao, wakaenda Ikonio. 52 Na wanafunzi walijaa furaha na Roho Mtakatifu.

Matendo ya Mitume 14

1 Ikawa huko Ikonio wakaingia pamoja katika sinagogi la Wayahudi; na kwa vile walivyonena, kundi kubwa la Wayahudi na la Wayunani wakaamini. 2 Walakini Wayahudi wasioamini wakawataharakisha watu wa Mataifa na kuwatia nia mbaya juu ya ndugu. 3 Basi wakakaa huko wakati mwingi, wakinena kwa ushujaa katika Bwana, aliyelishuhudia neno la neema yake, akiwajalia ishara na maajabu yatendeke kwa mikono yao. 4 Lakini jamii ya watu wa mjini wakafarakana; hawa walikuwa upande wa Wayahudi, na hawa upande wa Mitume. 5 Hata palipotokea shambulio la watu wa Mataifa na Wayahudi pamoja na wakubwa wao juu yao, kuwatenda jeuri na kuwapiga kwa mawe, 6 wao wakapata habari wakakimbilia Listra na Derbe, miji ya Likaonia, na nchi zilizo kando kando; 7 wakakaa huko, wakiihubiri Injili. 8 Na huko Listra palikuwa na mtu mmoja, dhaifu wa miguu, kiwete tangu tumboni mwa mamaye, ambaye hajaenda kabisa. 9 Mtu huyo alimsikia Paulo alipokuwa akinena; ambaye akamkazia macho na kuona ya kuwa ana imani ya kuponywa, 10 akasema kwa sauti kuu, Simama kwa miguu yako sawasawa. Akasimama upesi akaenda. 11 Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. 12 Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji. 13 Kuhani wa Zeu ambaye hekalu lake lilikuwa mbele ya mji, akaleta ng'ombe na taji za maua hata malangoni, akitaka kutoa dhabihu pamoja na makutano. 14 Walakini mitume Barnaba na Paulo, walipopata habari, wakararua nguo zao, wakaenda mbio wakaingia katika makutano, wakipiga kelele, 15 wakisema, Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; 16 ambaye zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe. 17 Lakini hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha. 18 Na kwa maneno hayo wakawazuia makutano kwa shida, wasiwatolee dhabihu. 19 Lakini Wayahudi wakafika toka Antiokia na Ikonio, wakawashawishi makutano hata wakampiga kwa mawe Paulo, wakamburuta nje ya mji, wakidhania ya kuwa amekwisha kufa. 20 Lakini wanafunzi walipokuwa wakimzunguka pande zote, akasimama, akaingia ndani ya mji; na siku ya pili yake akatoka, akaenda zake pamoja na Barnaba mpaka Derbe. 21 Hata walipokwisha kuihubiri Injili katika mji ule, na kupata wanafunzi wengi, wakarejea mpaka Listra na Ikonio na Antiokia, 22 wakifanya imara roho za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile Imani, na ya kwamba imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi. 23 Na walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila kanisa, na kuomba pamoja na kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini. 24 Wakapita kati ya Pisidia wakaingia Pamfilia. 25 Na baada ya kuhubiri lile neno katika Perge wakatelemka mpaka Atalia. 26 Na kutoka huko wakaabiri kwenda Antiokia. Huko ndiko walikoombewa neema ya Mungu kwa ile kazi waliyokwisha kuitimiza. 27 Hata walipofika wakalikutanisha kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia Mataifa mlango wa imani. 28 Wakaketi huko wakati usiokuwa mchache, pamoja na wanafunzi.

Matendo ya Mitume 15

1 Wakashuka watu waliotoka Uyahudi wakawafundisha wale ndugu ya kwamba, Msipotahiriwa kama desturi ya Musa hamwezi kuokoka. 2 Basi baada ya Paulo na Barnaba kushindana na watu hawa na kuhojiana nao sana, ndugu wakaamuru kwamba Paulo na Barnaba na wengine miongoni mwao wapande kwenda Yerusalemu kwa mitume na wazee kwa habari ya swali hilo. 3 Basi, wakisafirishwa na kanisa, wakapita kati ya nchi ya Foinike na Samaria, wakitangaza habari za kuongoka kwao Mataifa; wakawafurahisha ndugu sana. 4 Walipofika Yerusalemu wakakaribishwa na kanisa na mitume na wazee, nao wakawaeleza mambo yote Mungu aliyoyafanya pamoja nao. 5 Lakini baadhi ya madhehebu ya Mafarisayo walioamini wakasimama wakisema, Ni lazima kuwatahiri na kuwaagiza kuishika torati ya Musa. 6 Mitume na wazee wakakusanyika wapate kulifikiri neno hilo. 7 Na baada ya hoja nyingi Petro akasimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa walisikie neno la Injili kwa kinywa changu, na kuliamini. 8 Na Mungu, ajuaye mioyo ya watu, akawashuhudia, akiwapa Roho Mtakatifu vile vile kama alivyotupa sisi; 9 wala hakufanya tofauti kati yetu sisi na wao, akiwasafisha mioyo yao kwa imani. 10 Basi sasa mbona mnamjaribu Mungu na kuweka kongwa juu ya shingo za wanafunzi, ambalo baba zetu wala sisi hatukuweza kulichukua. 11 Bali twaamini kwamba tutaokoka kwa neema ya Bwana Yesu vile vile kama wao. 12 Basi mkutano wote wakanyamaza, wakawasikiliza Barnaba na Paulo wakiwapasha habari za ishara na maajabu, ambayo Mungu aliyafanya kwa ujumbe wao katika Mataifa. 13 Na hao walipokwisha kunyamaza Yakobo akajibu, akisema, Ndugu zangu, nisikilizeni. 14 Simeoni ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake. 15 Na maneno ya manabii yapatana na hayo, kama ilivyoandikwa, 16 Baada ya mambo haya nitarejea, Nami nitaijenga tena nyumba ya Daudi iliyoanguka. Nitajenga tena maanguko yake, Nami nitaisimamisha; 17 Ili wanadamu waliosalia wamtafute Bwana, Na mataifa yote ambao jina langu limetajwa kwao; 18 Asema Bwana, ajulishaye hayo tangu milele. 19 Kwa sababu hiyo mimi naamua hivi; Tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika Mataifa; 20 bali tuwaandikie kwamba wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu. 21 Kwa maana tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila sabato katika masinagogi. 22 Basi ikawapendeza mitume na wazee na kanisa lote kuwachagua watu miongoni mwao na kuwapeleka Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba; nao ni hawa, Yuda aliyeitwa Barsaba, na Sila, waliokuwa watu wakuu katika ndugu. Wakaandika hivi na kupeleka kwa mikono yao, 23 Mitume na ndugu wazee, kwa ndugu zetu walioko Antiokia na Shamu na Kilikia, walio wa Mataifa; Salamu. 24 Kwa kuwa tumesikia ya kwamba watu waliotoka kwetu wamewasumbua kwa maneno yao, wakipotosha roho zenu, ambao sisi hatukuwaagiza; 25 sisi tumeona vema, hali tumepatana kwa moyo mmoja, kuwachagua watu na kuwapeleka kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo, 26 watu waliohatirisha maisha yao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo. 27 Basi tumewatuma Yuda na Sila, watakaowaambia wenyewe maneno yayo hayo kwa vinywa vyao. 28 Kwa maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima, 29 yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati. Mkijizuia na hayo, mtafanya vema. Wasalamu. 30 Hata hao wakiisha kupewa ruhusa wakatelemkia Antiokia; na baada ya kuwakusanya jamii yote wakawapa ile barua. 31 Nao walipokwisha kuisoma wakafurahi kwa ajili ya faraja ile. 32 Tena Yuda na Sila, kwa kuwa wao wenyewe ni manabii, wakawausia ndugu kwa maneno mengi, wakawathibitisha. 33 Na wakiisha kukaa huko muda, wakaruhusiwa na ndugu waende kwa amani kwa hao waliowatuma. 34 Lakini Sila akaona vema kukaa huko. 35 Na Paulo na Barnaba wakakaa huko Antiokia, wakifundisha na kulihubiri neno la Bwana, pamoja na watu wengine wengi. 36 Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! Mrejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la Bwana, wa hali gani. 37 Barnaba akaazimu kumchukua Yohana aliyeitwa Marko pamoja nao. 38 Bali Paulo hakuona vema kumchukua huyo aliyewaacha huko Pamfilia, asiende nao kazini. 39 Basi palitokea mashindano baina yao hata wakatengana. Barnaba akamchukua Marko akatweka kwenda Kipro. 40 Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana. 41 Akapita katika Shamu na Kilikia akiyathibitisha makanisa.

Matendo ya Mitume 16

1 Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. 2 Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio. 3 Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani. 4 Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. 5 Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku. 6 Wakapita katika nchi ya Frigia na Galatia, wakikatazwa na Roho Mtakatifu, wasilihubiri lile neno katika Asia. 7 Walipofika kukabili Misia wakajaribu kuenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, 8 wakapita Misia wakatelemkia Troa. 9 Paulo akatokewa na maono usiku; alimwona mtu wa Makedonia amesimama, akimsihi, na kumwambia, Vuka, uje Makedonia utusaidie. 10 Basi alipokwisha kuyaona yale maono, mara tukataka kutoka kwenda Makedonia, kwa kuwa tuliona hakika ya kwamba Mungu ametuita tuwahubiri Habari Njema. 11 Basi tukang'oa nanga kutoka Troa, tukafika Samothrake kwa tanga moja, na siku ya pili tukafika Neapoli; 12 na kutoka hapo tukafika Filipi, mji wa Makedonia, mji ulio mkuu katika jimbo lile, mahali walipohamia Warumi; tukawa katika mji huu, tukikaa siku kadha wa kadha. 13 Hata siku ya sabato tukatoka nje ya lango, tukaenda kando ya mto, ambapo tukadhani ya kuwa pana mahali pa kusali; tukaketi, tukasema na wanawake waliokutana pale. 14 Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo. 15 Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake, akatusihi, akisema, Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani mwangu mkakae. Akatushurutisha. 16 Ikawa tulipokuwa tukienda mahali pale pa kusali, kijakazi mmoja aliyekuwa na pepo wa uaguzi akatukuta, aliyewapatia bwana zake faida nyingi kwa kuagua. 17 Akamfuata Paulo na sisi akipiga kelele, akisema, Watu hawa ni watumishi wa Mungu aliye juu, wenye kuwahubiria njia ya wokovu. 18 Akafanya hayo siku nyingi. Lakini Paulo akasikitika, akageuka akamwambia yule pepo, Nakuamuru kwa jina la Yesu Kristo, mtoke huyu. Akamtoka saa ile ile. 19 Basi bwana zake walipoona ya kuwa tumaini la faida yao limewapotea, wakawakamata Paulo na Sila, wakawakokota mpaka sokoni mbele ya wakuu wa mji; 20 wakawachukua kwa makadhi, wakasema, Watu hawa wanachafua sana mji wetu, nao ni Wayahudi; 21 tena wanatangaza habari ya desturi zisizokuwa halali kwetu kuzipokea wala kuzifuata, kwa kuwa sisi tu Warumi. 22 Makutano wote wakaondoka wakawaendea, makadhi wakawavua nguo zao kwa nguvu, wakatoa amri wapigwe kwa bakora. 23 Na walipokwisha kuwapiga mapigo mengi, wakawatupa gerezani, wakamwamuru mlinzi wa gereza awalinde sana. 24 Naye akiisha kupata amri hii akawatupa katika chumba cha ndani, akawafunga miguu kwa mkatale. 25 Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. 26 Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa. 27 Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua, akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia. 28 Ila Paulo akapaza sauti yake kwa nguvu, akisema, Usijidhuru, kwa maana sisi sote tupo hapa. 29 Akataka taa ziletwe, akarukia ndani, akitetemeka kwa hofu, akawaangukia Paulo na Sila; 30 kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? 31 Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako. 32 Wakamwambia neno la Bwana, yeye na watu wote waliomo nyumbani mwake. 33 Akawakaribisha saa ile ile ya usiku, akawaosha mapigo yao, kisha akabatizwa, yeye na watu wake wote wakati uo huo. 34 Akawaleta juu nyumbani kwake, akawaandalia chakula, akafurahi sana, yeye na nyumba yake yote, maana amekwisha kumwamini Mungu. 35 Kulipopambauka makadhi wakawatuma wakubwa wa askari wakisema, Waacheni watu wale waende zao. 36 Yule mlinzi wa gereza akamwarifu Paulo maneno haya akisema, Makadhi wametuma watu ili mfunguliwe; basi, sasa tokeni nje, enendeni zenu kwa amani. 37 Paulo akawaambia, Wametupiga mbele ya watu wote bila kutuhukumu, na sisi tu Warumi, tena wametutupa gerezani; na sasa wanataka kututoa kwa siri? Sivyo, lakini na waje wenyewe wakatutoe. 38 Wakubwa wa askari wakawapasha makadhi habari za maneno haya; nao wakaogopa, waliposikia ya kwamba hao ni Warumi. 39 Wakaja wakawasihi; na walipokwisha kuwatoa nje, wakawaomba watoke katika mji ule. 40 Nao wakatoka gerezani wakaingia nyumbani mwa Lidia; na walipokwisha kuonana na ndugu wakawafariji, wakaenda zao.

Matendo ya Mitume 17

1 Wakiisha kupita kati ya Amfipoli na Apolonia wakafika Thesalonike, ambapo palikuwa na sinagogi la Wayahudi. 2 Na Paulo, kama ilivyokuwa desturi yake, akaingia mle walimo, akahojiana nao kwa maneno ya maandiko sabato tatu, 3 akiyafunua na kuwaeleza ya kwamba ilimpasa Kristo kuteswa, na kufufuka katika wafu; na ya kwamba, Yesu huyu ninayewapasha ninyi habari zake ndiye Kristo. 4 Wengine miongoni mwao wakaamini, wakashikamana na Paulo na Sila; na Wayunani waliomcha Mungu, wengi sana, na wanawake wenye cheo si wachache. 5 Na Wayahudi wakaona wivu, wakajitwalia watu kadha wa kadha katika watu ovyo wasio na sifa njema, nao wakakutanisha mkutano, wakafanya ghasia mjini, wakawaendea watu wa nyumba ya Yasoni, wakataka kuwapeleka mbele ya watu wa mji; 6 na walipowakosa, wakamkokota Yasoni na baadhi ya ndugu mbele ya wakubwa wa mji, wakipiga kelele, wakisema, Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako, 7 na Yasoni amewakaribisha; na hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema na kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu. 8 Wakafadhaisha ule mkutano na wakubwa wa mji walipoyasikia hayo. 9 Nao walipokwisha kumtoza dhamana Yasoni na wenziwe wakawaacha waende zao. 10 Mara hao ndugu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia katika sinagogi la Wayahudi. 11 Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo. 12 Basi watu wengi miongoni mwao wakaamini, na wanawake wa Kiyunani wenye cheo, na wanaume si wachache. 13 Lakini Wayahudi wa Thesalonike walipopata habari ya kwamba neno la Mungu linahubiriwa na Paulo hata katika Beroya, wakaenda huko nako wakawachafua na kuwafadhaisha makutano. 14 Mara hiyo wale ndugu wakampeleka Paulo aende zake mpaka pwani; bali Sila na Timotheo wakasalia huko. 15 Lakini wale waliomsindikiza Paulo wakampeleka mpaka Athene; nao wakiisha kupokea maagizo kuwapelekea Sila na Timotheo, ya kwamba wasikawie kumfuata, wakaenda zao. 16 Paulo alipokuwa akiwangojea huko Athene na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake. 17 Basi katika sinagogi akahojiana na Wayahudi na waliomcha Mungu, na wale waliokutana naye sokoni kila siku. 18 Na baadhi ya Waepikureo na Wastoiko, wenye ujuzi, wakakutana naye. Wengine wakasema, Mpuzi huyu anataka kusema nini? Wengine walisema, Anaonekana kuwa mtangaza habari za miungu migeni, kwa maana alikuwa akihubiri habari za Yesu na ufufuo. 19 Wakamshika, wakamchukua Areopago, wakisema, Je! Twaweza kujua maana ya elimu hii mpya unayoinena? 20 Kwa maana unaleta mambo mageni masikioni mwetu, tutapenda kujua, basi, maana ya mambo haya. 21 Kwa maana Waathene na wageni waliokaa huko walikuwa hawana nafasi kwa neno lo lote ila kutoa habari na kusikiliza habari za jambo jipya. 22 Paulo akasimama katikati ya Areopago, akasema, Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini. 23 Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, KWA MUNGU ASIYEJULIKANA. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua. 24 Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana wa mbingu na nchi, hakai katika hekalu zilizojengwa kwa mikono; 25 wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kana kwamba anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote. 26 Naye alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao; 27 ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu. 28 Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu. Kama vile mmoja wenu, mtunga mashairi alivyosema, Maana sisi sote tu wazao wake. 29 Basi, kwa kuwa sisi tu wazao wa Mungu, haitupasi kudhani ya kuwa Uungu ni mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu. 30 Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. 31 Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu. 32 Basi waliposikia habari za ufufuo wa wafu wengine walifanya dhihaka; wengine wakasema, Tutakusikiliza tena katika habari hiyo. 33 Basi hivi Paulo akaondoka akawaacha. 34 Baadhi ya watu wakashikamana naye, wakaamini; katika hao alikuwamo Dionisio, Mwareopago, na mwanamke mmoja jina lake Damari, na watu wengine pamoja na hao.

Matendo ya Mitume 18

1 Baada ya mambo hayo, Paulo akatoka Athene akafika Korintho. 2 Akamwona Myahudi mmoja, jina lake Akila, mzalia wa Ponto; naye amekuja kutoka nchi ya Italia siku za karibu, pamoja na Prisila mkewe, kwa sababu Klaudio amewaamuru Wayahudi wote watoke Rumi, naye akafikilia kwao; 3 na kwa kuwa kazi yao ya ufundi ilikuwa moja, akakaa kwao, wakafanya kazi pamoja, kwa maana walikuwa mafundi wa kushona hema. 4 Akatoa hoja zake katika sinagogi kila sabato, akajaribu kuwavuta Wayahudi na Wayunani. 5 Hata Sila na Timotheo walipotelemka kutoka Makedonia, Paulo akasongwa sana na lile neno, akiwashuhudia Wayahudi ya kwamba Yesu ni Kristo. 6 Walipopingamana naye na kumtukana Mungu, akakung'uta mavazi yake, akawaambia, Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu; mimi ni safi; tangu sasa nitakwenda kwa watu wa Mataifa. 7 Akaondoka huko akaingia katika nyumba ya mtu mmoja jina lake Tito Yusto, mcha Mungu, ambaye nyumba yake ilikuwa mpaka mmoja na sinagogi. 8 Na Krispo, mkuu wa sinagogi, akamwamini Bwana pamoja na nyumba yake yote. Wakorintho wengi waliposikia, waliamini, wakabatizwa. 9 Bwana akamwambia Paulo kwa maono usiku, Usiogope, bali nena, wala usinyamaze, 10 kwa kuwa mimi ni pamoja nawe, wala hapana mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana mimi nina watu wengi katika mji huu. 11 Akakaa huko muda wa mwaka mmoja na miezi sita akifundisha kati yao neno la Mungu. 12 Hata Galio alipokuwa liwali wa Akaya, Wayahudi wakamwinukia Paulo kwa nia moja, wakamleta mbele ya kiti cha hukumu, 13 wakisema Mtu huyu huwavuta watu ili wamwabudu Mungu kinyume cha sheria. 14 Na Paulo alipotaka kufunua kinywa chake, Galio akawaambia Wayahudi, Kama lingekuwa jambo la dhuluma au la hila mbaya, enyi Wayahudi, ingekuwa haki mimi kuchukuliana nanyi; 15 bali ikiwa ni hoja juu ya maneno na majina na sheria yenu, liangalieni ninyi wenyewe, maana mimi sitaki kuwa mwamuzi wa mambo hayo. 16 Akawafukuza waondoke mbele ya kiti cha hukumu. 17 Nao wote wakamshika Sosthene, mkuu wa sinagogi, wakampiga mbele ya kiti cha hukumu. Wala Galio hakuyaona mambo hayo kuwa ni kitu. 18 Baada ya hayo Paulo akazidi kukaa huko siku nyingi, kisha akaagana na ndugu akaabiri kwenda Shamu; na Prisila na Akila wakaenda pamoja naye, alipokwisha kunyoa kichwa chake huko Kenkrea; maana alikuwa ana nadhiri. 19 Wakafika Efeso, akawaacha huko. Yeye mwenyewe akaingia katika sinagogi, akahojiana na Wayahudi. 20 Walipomtaka akae wakati mwingi zaidi, hakukubali; 21 bali aliagana nao, akisema, Nitarejea kwenu tena, Mungu akinijalia. Akatweka, akatoka Efeso, 22 na alipokwisha kushuka Kaisaria, akapanda juu, akawasalimu kanisa, kisha akatelemkia Antiokia. 23 Hata akiisha kukaa huko siku kadha wa kadha akaondoka, akapita kati ya nchi ya Galatia na Frigia, mji kwa mji, akiwathibitisha wanafunzi. 24 Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. 25 Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu. 26 Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi. 27 Na alipotaka kuvuka bahari aende mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe, naye alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu. 28 Kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.

Matendo ya Mitume 19

1 Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; 2 akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. 3 Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. 4 Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. 5 Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. 6 Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri. 7 Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili. 8 Akaingia ndani ya sinagogi, akanena kwa ushujaa kwa muda wa miezi mitatu, akihojiana na watu, na kuwavuta katika mambo ya ufalme wa Mungu. 9 Lakini wengine walikaidi, wakakataa kuamini, wakiitukana ile Njia mbele ya mkutano; basi, akaondoka akawaacha, akawatenga wanafunzi, akahojiana na watu kila siku katika darasa ya mtu mmoja, jina lake Tirano. 10 Mambo haya yakaendelea kwa muda wa miaka miwili, hata wote waliokaa Asia wakalisikia neno la Bwana, Wayahudi kwa Wayunani. 11 Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida; 12 hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawaondokea, pepo wachafu wakawatoka. 13 Baadhi ya Wayahudi wenye kutanga-tanga, nao ni wapunga pepo, wakajaribu kutaja jina la Bwana Yesu juu yao waliopagawa na pepo wachafu, wakisema, Nawaapisha kwa Yesu, yule anayehubiriwa na Paulo. 14 Walikuwako wana saba wa mtu mmoja Skewa, Myahudi, kuhani mkuu, waliofanya hivyo. 15 Yule pepo mchafu akawajibu, akawaambia, Yesu namjua na Paulo namfahamu, lakini ninyi ni nani? 16 Na yule mtu aliyepagawa na pepo mchafu akawarukia wawili, akawaweza, akawashinda, hata wakatoka mbio katika nyumba ile hali wa uchi na kujeruhiwa. 17 Habari hii ikajulikana na Wayahudi wote na Wayunani waliokaa Efeso, hofu ikawaingia wote, na jina la Bwana Yesu likatukuzwa. 18 Na wengi wa wale walioamini wakaja wakaungama, wakidhihirisha matendo yao. 19 Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu. 20 Hivyo ndivyo neno la Bwana lilivyozidi na kushinda kwa nguvu. 21 Mambo hayo yalipokwisha kumalizika, Paulo akaazimu rohoni mwake, akiisha kupita katika Makedonia na Akaya, aende Yerusalemu, akisema, Baada ya kuwako huko, yanipasa kuuona na Rumi pia. 22 Akatuma watu wawili miongoni mwa wale waliomtumikia kwenda Makedonia, nao ni Timotheo na Erasto, yeye mwenyewe akakaa katika Asia kitambo. 23 Wakati huo kukatukia ghasia si haba katika habari ya Njia ile. 24 Kwa maana mtu mmoja, jina lake Demetrio, mfua fedha, aliyekuwa akifanya vihekalu vya fedha vya Artemi, alikuwa akiwapatia mafundi faida nyingi. 25 Akawakusanya hao, pamoja na wengine wenye kazi ile ile, akasema, Enyi wanaume, mnajua ya kuwa utajiri wetu hutoka katika kazi hii. 26 Tena mnaona na kusikia ya kwamba si katika Efeso tu, bali katika Asia yote pia Paulo huyo ameshawishi watu wengi na kuwageuza nia zao, akisema ya kwamba hiyo inayofanywa kwa mikono siyo miungu. 27 Si kwamba kazi hii yetu ina hatari ya kudharauliwa tu; bali na hekalu la mungu mke aliye mkuu, Artemi, kuhesabiwa si kitu, na kuondolewa utukufu wake, ambaye Asia yote pia na walimwengu wote humwabudu. 28 Waliposikia haya wakajaa ghadhabu, wakapiga kelele, wakisema, Artemi wa Waefeso ni mkuu. 29 Mji wote ukajaa ghasia, wakaenda mbio wakaingia mahali pa michezo kwa nia moja, wakiisha kuwakamata Gayo na Aristarko, watu wa Makedonia waliosafiri pamoja na Paulo. 30 Na Paulo alipotaka kuingia kati ya watu, wanafunzi hawakumwacha aingie. 31 Na baadhi ya wakuu wa Asia, walio rafiki zake, wakatuma watu kwake, wakimsihi asijihudhurishe nafsi yake ndani ya mahali pa michezo. 32 Basi wengine walikuwa wakilia hivi na wengine hivi; kwa maana ule mkutano ulikuwa umechafuka-chafuka, na wengi wao hawakuijua sababu ya kukusanyika kwao pamoja. 33 Wakamtoa Iskanda katika mkutano, Wayahudi wakimweka mbele ya watu. Iskanda akawapungia mkono, akitaka kujitetea mbele ya wale watu. 34 Lakini walipotambua ya kuwa yeye ni Myahudi, wakapiga kelele wote pia kwa sauti moja kwa muda wa kama saa mbili, wakisema, Artemi wa Waefeso ni mkuu. 35 Na karani wa mji alipokwisha kuwatuliza watu, akasema, Enyi wanaume wa Efeso, ni mtu gani asiyejua ya kuwa mji wa Efeso ni mtunzaji wa hekalu la Artemi, aliye mkuu, na wa kitu kile kilichoanguka kutoka mbinguni? 36 Basi kwa kuwa mambo haya hayawezi kukanushwa, imewapasa kutulia; msifanye neno la haraka haraka. 37 Kwa maana mmewaleta watu hawa, wasioiba vitu vya hekalu wala kumtukana mungu mke wetu. 38 Basi ikiwa Demetrio na mafundi walio pamoja naye wana neno juu ya mtu, baraza ziko, na maliwali wako; na washitakiane. 39 Bali mkitafuta neno lo lote katika mambo mengine, yatatengenezwa katika kusanyiko lililo halali. 40 Kwa maana tuna hatari ya kushitakiwa kwa ajili ya matata haya ya leo, ambayo hayana sababu; na katika neno hilo, hatutaweza kujiudhuru kwa mkutano huu. 41 Alipokwisha kusema haya akauvunja mkutano.

Matendo ya Mitume 20

1 Kishindo kile kilipokoma, Paulo akatuma kuwaita wanafunzi akawaonya, akaagana nao, kisha akaondoka aende zake mpaka Makedonia. 2 Naye akiisha kupita pande zile na kuwafariji kwa maneno mengi, akafika Uyunani. 3 Alipokwisha kukaa huko miezi mitatu, na Wayahudi kumfanyia vitimvi, alipotaka kwenda Shamu kwa njia ya bahari; basi akaazimu kurejea kwa njia ya Makedonia. 4 Watu hawa wakafuatana naye, Sopatro Mberoya, mwana wa Piro, na Aristarko na Sekundo, watu wa Thesalonike; na Gayo mtu wa Derbe, na Timotheo; na Tikiko na Trofimo watu wa Asia. 5 Ila watu hao wamekwisha kutangulia wakamngojea Troa. 6 Sisi tukatweka baada ya siku za mikate isiyotiwa chachu, tukatoka Filipi, tukawafikia Troa, safari ya siku tano, tukakaa huko siku saba. 7 Hata siku ya kwanza ya juma, tulipokuwa tumekutana ili kumega mkate, Paulo akawahutubu, akiazimu kusafiri siku ya pili yake, naye akafuliza maneno yake hata usiku wa manane. 8 Palikuwa na taa nyingi katika orofa ile tulipokuwa tumekusanyika. 9 Kijana mmoja, jina lake Eutiko, alikuwa ameketi dirishani, akalemewa na usingizi sana; hata Paulo alipoendelea sana kuhubiri, akazidiwa na usingizi wake akaanguka toka orofa ya tatu; akainuliwa amekwisha kufa. 10 Paulo akashuka, akamwangukia, akamkumbatia, akasema, Msifanye ghasia, maana uzima wake ungalimo ndani yake. 11 Akapanda juu tena, akamega mkate, akala, akazidi kuongea nao hata alfajiri, ndipo akaenda zake. 12 Wakamleta yule kijana, yu mzima, wakafarijika faraja kubwa sana. 13 Lakini sisi tukatangulia kwenda merikebuni, tukaabiri kwenda Aso, tukikusudia kumpakia Paulo huko; kwa maana ndivyo alivyoagiza, yeye mwenyewe aliazimu kwenda kwa miguu. 14 Alipotufikia huko Aso, tukampakia, kisha tukafika Mitilene. 15 Tukatweka kutoka huko, na siku ya pili tukafika mahali panapokabili Kio; siku ya tatu tukawasili Samo, tukakaa Trogilio, siku ya nne tukafika Mileto. 16 Kwa sababu Paulo amekusudia kupita Efeso merikebuni, asije akakawia katika Asia; kwa maana alikuwa na haraka, akitaka kuwahi Yerusalemu siku ya Pentekoste, kama ikiwezekana. 17 Toka Mileto Paulo akatuma watu kwenda Efeso, akawaita wazee wa kanisa. 18 Walipofika kwake, akawaambia, Ninyi wenyewe mnajua tangu siku ya kwanza nilipokanyaga hapa Asia, jinsi nilivyokuwa kwenu wakati wote, 19 nikimtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi, na majaribu yaliyonipata kwa hila za Wayahudi; 20 ya kuwa sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba, 21 nikiwashuhudia Wayahudi na Wayunani wamtubie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo. 22 Basi sasa, angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni, nisiyajue mambo yatakayonikuta huko; 23 isipokuwa Roho Mtakatifu mji kwa mji hunishuhudia akisema, ya kwamba vifungo na dhiki vyaningoja. 24 Lakini siyahesabu maisha yangu kuwa kitu cha thamani kwangu kama kuumaliza mwendo wangu na huduma ile niliyopokea kwa Bwana Yesu, kuishuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu. 25 Na sasa, tazameni, mimi najua ya kuwa ninyi nyote niliowahubiria ufalme wa Mungu, nikienda huko na huko, hamtaniona uso tena. 26 Kwa hiyo nawashuhudia wote siku hii ya leo, ya kuwa mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. 27 Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu. 28 Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe. 29 Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; 30 tena katika ninyi wenyewe watainuka watu wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao. 31 Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi. 32 Basi, sasa nawaweka katika mikono ya Mungu, na kwa neno la neema yake, ambalo laweza kuwajenga na kuwapa urithi pamoja nao wote waliotakaswa. 33 Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. 34 Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. 35 Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea. 36 Alipokwisha kunena haya akapiga magoti, akaomba pamoja nao wote. 37 Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu, 38 wakihuzunika zaidi kwa sababu ya neno lile alilosema, ya kwamba hawatamwona uso tena. Wakamsindikiza hata merikebuni.

Matendo ya Mitume 21

1 Ikawa tulipokwisha kujitenga nao na kuabiri, tukafika Kosi kwa tanga moja, na siku ya pili yake tukafika Rodo na kutoka huko tukafika Patara, 2 tukapata merikebu itakayovuka mpaka Foinike tukapanda tukatweka. 3 Na tulipoona Kipro tukaiacha upande wa kushoto; tukasafiri mpaka Shamu tukashuka Tiro. Kwa maana huko ndiko merikebu yetu itakakoshusha shehena yake. 4 Tukiisha kuwaona wanafunzi tukakaa huko siku saba, nao wakamwambia Paulo kwa uweza wa Roho asipande kwenda Yerusalemu. 5 Hata tulipotimiza siku zile tukaondoka tukaenda zetu, na watu wote, pamoja na wake zao na watoto wao, wakatusindikiza mpake nje ya mji, tukapiga magoti pwani tukaomba; 6 na baada ya kuagana tukapanda merikebuni, nao wakarudi kwao. 7 Hata tulipomaliza safari yetu kutoka Tiro tukafika Tolemai, tukawaamkua ndugu tukakaa kwao siku moja. 8 Asubuhi yake tukaondoka, tukafika Kaisaria, tukaingia nyumbani mwa Filipo, mhubiri wa Injili, aliyekuwa mmoja wa wale saba, tukakaa kwake. 9 Mtu huyu alikuwa na binti wanne, mabikira, waliokuwa wakitabiri. 10 Basi tulipokuwa tukikaa huko siku nyingi, nabii mmoja jina lake Agabo akashuka kutoka Uyahudi. 11 Alipotufikia akautwaa mshipi wa Paulo, akajifunga miguu na mikono, akasema, Roho Mtakatifu asema hivi, Hivyo ndivyo Wayahudi wa Yerusalemu watakavyomfunga mtu mwenye mshipi huu, nao watamtia katika mikono ya watu wa Mataifa. 12 Basi tuliposikia haya, sisi na watu wa mahali pale, tukamsihi asipande kwenda Yerusalemu. 13 Ndipo Paulo alipojibu, Mnafanya nini, kulia na kunivunja moyo? Kwa maana mimi, licha ya kufungwa, ni tayari hata kuuawa katika Yerusalemu kwa ajili ya jina lake Bwana Yesu. 14 Alipokataa shauri letu, tukanyamaza tukisema, Mapenzi ya Bwana na yatendeke. 15 Baada ya siku zile tukachukua vyombo vyetu tukapanda kwenda Yerusalemu. 16 Baadhi ya wanafunzi wa Kaisaria wakafuatana na sisi, wakamchukua na Mnasoni, mtu wa Kipro, mwanafunzi wa zamani ambaye ndiye tutakayekaa kwake. 17 Tulipofika Yerusalemu wale ndugu wakatukaribisha kwa furaha. 18 Hata siku ya pili yake Paulo akaingia kwa Yakobo pamoja nasi, na wazee wote walikuwako. 19 Na baada ya kuwaamkua, akawaeleza mambo yote moja moja Mungu aliyoyatenda katika Mataifa kwa huduma yake. 20 Nao waliposikia wakamtukuza Mungu, wakamwambia, Ndugu yetu, unaona jinsi Wayahudi walioamini walivyo elfu nyingi, nao wote wana wivu sana kwa ajili ya torati. 21 Nao wameambiwa habari zako, ya kwamba unawafundisha Wayahudi wote wakaao katika Mataifa kumwacha Musa, ukiwaambia wasiwatahiri watoto wao, wala wasizifuate desturi. 22 Basi, ni nini? Bila shaka watasikia kwamba umekuja. 23 Basi fanya neno hili tunalokuambia. Wako kwetu watu wanne waliofungwa na nadhiri. 24 Wachukue watu hao, ujitakase pamoja nao, na kuwagharimia ili wanyoe vichwa vyao, watu wote wapate kujua ya kuwa habari zile walizoambiwa juu yako si kitu, bali wewe mwenyewe unaenenda vizuri na kuishika torati. 25 Lakini kwa habari za watu wa Mataifa walioamini, tuliandika na kutoa hukumu yetu ya wao kujilinda nafsi zao na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na kitu kilichosongolewa, na uasherati. 26 Ndipo Paulo akawatwaa wanaume wale, na siku ya pili yake akajitakasa nafsi yake pamoja nao, akaingia ndani ya hekalu, akitangaza habari ya kutimiza siku za utakaso, hata sadaka itolewe kwa ajili ya kila mmoja wao. 27 Basi zile siku saba zilipokuwa karibu kutimia, Wayahudi waliotoka Asia wakamwona ndani ya hekalu, wakawataharakisha watu wote, wakamkamata, 28 wakapiga kelele, na kusema, Enyi wanaume wa Israeli, tusaidieni. Huyu ndiye mtu yule afundishaye watu wote kila mahali kinyume cha taifa letu na torati na mahali hapa. Tena, zaidi ya haya, amewaingiza Wayunani katika hekalu, akapatia unajisi mahali hapa patakatifu. 29 Kwa maana walikuwa wamemwona Trofimo, Mwefeso, pamoja naye mjini, ambaye walidhania ya kuwa Paulo amemwingiza katika hekalu. 30 Mji wote ukataharuki, watu wakakutanika mbio mbio, wakamkamata Paulo, wakamkokota, wakamtoa hekaluni; mara milango ikafungwa. 31 Na walipokuwa wakitafuta njia ya kumwua, habari zikamfikilia jemadari wa kikosi ya kwamba Yerusalemu imechafuka, mji mzima. 32 Mara akatwaa askari na maakida, akawashukia mbio. Nao walipomwona jemadari na askari wakaacha kumpiga Paulo. 33 Kisha jemadari akakaribia, akamshika, akaamuru afungwe kwa minyororo miwili; akauliza, Nani huyu? Tena, amefanya nini? 34 Wengine katika makutano wakapiga kelele wakisema hivi, na wengine hivi. Basi alipokuwa hawezi kupata hakika ya habari kwa sababu ya zile kelele, akatoa amri aletwe ndani ya ngome. 35 Basi Paulo alipofika darajani ilikuwa kuchukuliwa na askari kwa sababu ya nguvu ya makutano. 36 Maana kundi kubwa la watu wakamfuata, wakipiga kelele, na kusema, Mwondoe huyu. 37 Naye alipokuwa analetwa ndani ya ngome, Paulo akamwambia jemadari, Nina ruhusa nikuambie neno? Naye akasema, Je! Unajua Kiyunani? 38 Wewe si yule Mmisri ambaye kabla ya siku hizi aliwafitinisha wale watu elfu nne, walioitwa Wauaji, akawaongoza jangwani? 39 Paulo akasema, Mimi ni mtu wa Kiyahudi, mtu wa Tarso, mji wa Kilikia, mwenyeji wa mji usiokuwa mnyonge. Nakuomba, nipe ruhusa niseme na wenyeji hawa. 40 Basi, alipompa ruhusa, Paulo akasimama madarajani, akawapungia mkono wale wenyeji; na ilipokuwa kimya kabisa, akanena nao kwa lugha ya Kiebrania, akisema,

Matendo ya Mitume 22

1 Enyi wanaume, ndugu zangu na baba zangu, nisikilizeni, nikijitetea mbele yenu sasa. 2 Waliposikia kwamba anasema nao kwa lugha ya Kiebrania wakazidi kunyamaza; akasema, 3 Mimi ni mtu wa Kiyahudi, nalizaliwa Tarso, mji wa Kilikia, ila nililelewa katika mji huu, miguuni pa Gamalieli, nikafundishwa sheria ya baba zetu kwa usahihi, nikawa mtu wa jitihadi kwa Mungu kama ninyi nyote mlivyo leo hivi; 4 nikawaudhi watu wa Njia hii hata kuwaua, nikawafunga, nikiwatia gerezani, wanaume na wanawake. 5 Kama Kuhani Mkuu naye anishuhudiavyo, na wazee wa baraza wote pia, ambao nalipokea barua kwao kuwapelekea ndugu wale, nikaenda Dameski, ili niwalete wale waliokuwa huko hata Yerusalemu, hali wamefungwa, ili waadhibiwe. 6 Ikawa nilipokuwa nikisafiri, nikikaribia Dameski, wakati wa adhuhuri, ghafula nuru kuu ilitoka mbinguni, ikanimulikia pande zote. 7 Nikaanguka nchi, nikasikia sauti ikiniambia, Sauli, Sauli, mbona unaniudhi? 8 Nikajibu, Wewe u nani, Bwana? Akaniambia, Mimi ni Yesu Mnazareti, ambaye wewe unaniudhi. 9 Na wale waliokuwa pamoja nami waliiona ile nuru, lakini hawakuisikia ile sauti ya yule aliyesema nami. 10 Nikasema, Nifanye nini, Bwana? Bwana akaniambia, Simama, uingie Dameski, na huko utaambiwa habari za mambo yote yaliyoamriwa uyafanye. 11 Na nilipokuwa sioni kwa sababu ya fahari ya nuru ile, nikaongozwa na mikono yao waliokuwa pamoja nami, nikaingia Dameski. 12 Basi mtu mmoja, Anania, mtauwa kwa kuifuata sheria, aliyeshuhudiwa wema na Wayahudi wote waliokaa huko, 13 Akanijia, akasimama karibu nami, akaniambia, Ndugu yangu Sauli, uone. Nikamwinulia macho yangu saa ile ile. 14 Akasema, Mungu wa baba zetu amekuchagua wewe upate kujua mapenzi yake, na kumwona yule Mwenye haki, na kuisikia sauti itokayo katika kinywa chake. 15 Kwa maana utakuwa shahidi wake kwa watu wote, wa mambo hayo uliyoyaona na kuyasikia. 16 Basi sasa, unakawilia nini? Simama, ubatizwe, ukaoshe dhambi zako, ukiliitia jina lake. 17 Ikawa nilipokwisha kurudi Yerusalemu, nilipokuwa nikisali ndani ya hekalu, nikawa hali ya kuzimia roho, 18 nikamwona, naye akiniambia, Hima, utoke Yerusalemu upesi, kwa sababu hawatakubali ushuhuda wako katika habari zangu. 19 Nami nikasema, Bwana, wanajua hao ya kuwa mimi nalikuwa nikiwafunga gerezani wale wanaokuamini na kuwapiga katika kila sinagogi. 20 Na damu ya Stefano shahidi wako ilipomwagwa, mimi nami nilikuwa nikisimama karibu, nikikubali, na kuzitunza nguo zao waliomwua. 21 Naye akaniambia, Enenda zako; kwa kuwa mimi nitakutuma uende mbali kwa watu wa Mataifa. 22 Wakamsikiliza mpaka neno lile, wakapaza sauti zao, wakisema, Mwondoe huyu katika nchi, kwa maana haifai aishi. 23 Walipokuwa wakipiga kelele na kutupa mavazi yao na kurusha-rusha mavumbi juu, 24 yule jemadari akaamuru aletwe ndani ya ngome, akisema aulizwe habari zake kwa kupigwa mijeledi, ili ajue sababu hata wakampigia kelele namna hii. 25 Hata walipokwisha kumfunga kwa kamba, Paulo akamwambia yule akida aliyesimama karibu, Je! Ni halali ninyi kumpiga mtu aliye Mrumi naye hajakuhumiwa bado? 26 Yule akida aliposikia, akaenda akamwarifu yule jemadari, akisema, Unataka kufanya nini? Kwa maana mtu huyu ni Mrumi. 27 Jemadari akaja, akamwuliza, Niambie, u Mrumi? Akasema, Ndiyo. 28 Jemadari akajibu, Mimi nalipata wenyeji huu kwa mali nyingi. Paulo akasema, Na mimi ni Mrumi wa kuzaliwa. 29 Basi wale waliokuwa tayari kumwuliza wakaondoka wakamwacha. Na yule jemadari naye akaogopa, alipojua ya kuwa ni Mrumi, na kwa sababu amemfunga. 30 Siku ya pili yake akitaka kujua hakika, ni kwa sababu gani ameshitakiwa na Wayahudi, akamfungua, akawaamuru wakuu wa makuhani na baraza yote wakutane. Akamleta Paulo chini, akamweka mbele yao.

Matendo ya Mitume 23

1 Paulo akawakazia macho watu wa baraza, akasema, Ndugu zangu, mimi kwa dhamiri safi kabisa nimeishi mbele za Mungu hata leo hivi. 2 Kuhani Mkuu Anania akawaamuru wale waliosimama karibu naye wampige kinywa chake. 3 Ndipo Paulo akamwambia, Mungu atakupiga wewe, ukuta uliopakwa chokaa. Wewe umeketi kunihukumu sawasawa na sheria, nawe unaamuru nipigwe kinyume cha sheria? 4 Wale waliosimama karibu wakasema, Je! Unamtukana Kuhani Mkuu wa Mungu? 5 Paulo akasema, Sikujua, ndugu zangu, ya kuwa yeye ni Kuhani Mkuu; maana imeandikwa, Usimnenee mabaya mkuu wa watu wako. 6 Paulo alipotambua ya kuwa sehemu moja ni Masadukayo, na sehemu ya pili ni Mafarisayo, akapaza sauti yake katika ile baraza, Ndugu zangu, mimi ni Farisayo mwana wa Farisayo; mimi ninahukumiwa kwa ajili ya tumaini la ufufuo wa wafu. 7 Alipokwisha kunena hayo palikuwa na mashindano baina ya Mafarisayo na Masadukayo, mkutano ukafarakana. 8 Kwa maana Masadukayo husema ya kwamba hakuna kiyama wala malaika wala roho; bali Mafarisayo hukiri yote. 9 Pakawa na makelele mengi. Waandishi wengine wa upande wa Mafarisayo wakasimama, wakateta, wakisema, Hatuoni uovu wo wote katika mtu huyu; bali ikiwa roho au malaika amesema naye, ni nini? 10 Ugomvi mkubwa ulipotokea, yule jemadari akachelea Paulo asije akararuliwa nao, akaamuru askari washuke na kumwondoa kwa nguvu mikononi mwao, na kumleta ndani ya ngome. 11 Usiku ule Bwana akasimama karibu naye, akasema, Uwe na moyo mkuu; kwa sababu, kama ulivyonishuhudia habari zangu Yerusalemu, imekupasa kunishuhudia vivyo hivyo Rumi nako. 12 Kulipopambauka, Wayahudi wakafanya mapatano, wakajifunga kwa kiapo kwamba hawatakula wala hawatakunywa hata wamwue Paulo. 13 Na hao walioapiana hivyo walipata zaidi ya watu arobaini. 14 Nao wakaenda kwa wakuu wa makuhani na wazee, wakasema, Tumejifunga kwa kiapo tusionje kitu hata tumwue Paulo. 15 Basi sasa ninyi pamoja na wazee wa baraza mwambieni jemadari amlete chini kwenu, kana kwamba mnataka kujua habari zake vizuri zaidi; na sisi tu tayari kumwua kabla hajakaribia. 16 Mjomba wake Paulo akasikia habari za kuotea kwao, akaenda akaingia ndani ya ngome akampasha Paulo habari. 17 Paulo akamwita akida mmoja, akasema, Mchukue kijana huyu kwa jemadari; maana ana neno la kumwarifu. 18 Basi akamchukua, akampeleka kwa jemadari, akamwambia, Paulo, yule mfungwa, aliniita akataka nikuletee kijana huyu kwa kuwa ana neno la kukuambia. 19 Yule jemadari akamshika mkono akajitenga pamoja naye kando, akamwuliza kwa faragha, Una neno gani utakalo kuniarifu? 20 Akasema Wayahudi wamepatana kukuomba umlete Paulo chini kesho, ukamweke mbele ya baraza, kana kwamba wanataka kupata habari zake kwa usahihi zaidi. 21 Basi wewe usikubali; kwa maana watu zaidi ya arobaini wanamwotea, wamejifunga kwa kiapo wasile wala wasinywe hata watakapomwua; nao sasa wako tayari, wakiitazamia ahadi kwako. 22 Basi yule jemadari akamwacha kijana aende zake, akimwagiza, Usimwambie mtu awaye yote ya kwamba umeniarifu haya. 23 Akawaita maakida wawili, akasema, Wekeni tayari askari mia mbili kwenda Kaisaria, na askari wapanda farasi sabini, na wenye mikuki mia mbili, kwa saa tatu ya usiku. 24 Akawaambia kuweka wanyama tayari wampandishe Paulo, na kumchukua salama kwa Feliki liwali. 25 Akaandika barua, kwa namna hii, 26 Klaudio Lisia kwa liwali mtukufu Feliki, Salamu! 27 Mtu huyu alikamatwa na Wayahudi, wakawa karibu kumwua, ndipo nikaenda pamoja na kikosi cha askari nikamwokoa, nilipopata habari ya kuwa yeye ni Mrumi. 28 Nami nikitaka kulijua lile neno walilomshitakia, nikamtelemsha nikamweka mbele ya baraza; 29 nikaona kwamba ameshitakiwa kwa ajili ya maswali ya sheria yao, wala hakushitakiwa neno lo lote la kustahili kuuawa wala kufungwa. 30 Hata nilipopewa habari kwamba patakuwa na vitimvi juu ya mtu huyu, mara nikampeleka kwako, nikawaagiza na wale waliomshitaki, wanene habari zake mbele yako. Wasalamu. 31 Basi, wale askari wakamchukua Paulo kama walivyoamriwa, wakampeleka hata Antipatri usiku; 32 hata asubuhi wakawaacha wale wapanda farasi waende pamoja naye, nao wakarudi zao ngomeni. 33 Na wale walipofika Kaisaria, na kumpa liwali ile barua, wakamweka Paulo mbele yake. 34 Naye alipokwisha kuisoma, akawauliza, Mtu huyu ni wa jimbo gani? Alipoarifiwa ya kuwa ni mtu wa Kilikia, 35 akasema, Nitakusikia wewe watakapokuja wale waliokushitaki; akaamuru alindwe katika nyumba ya uliwali ya Herode.

Matendo ya Mitume 24

1 Baada ya siku tano, Anania, Kuhani Mkuu, akatelemka na baadhi ya wazee pamoja naye, na msemi mmoja, Tertulo, nao wakamweleza liwali habari za Paulo. 2 Naye alipoitwa, Tertulo akaanza kumshitaki, akisema, Kwa kuwa mnapata amani nyingi chini yako, Feliki mtukufu, na kwa maangalizi yako mambo mabaya yanatengenezwa kwa ajili ya taifa hili, 3 basi tunayapokea kila wakati na kila mahali, kwa shukrani yote. 4 Lakini nisikuudhi zaidi, nakusihi utusikilize maneno machache kwa fadhili zako. 5 Kwa maana tumemwona mtu huyu mkorofi, mwanzilishi wa fitina katika Wayahudi wote duniani, tena ni kichwa cha madhehebu ya Wanazorayo. 6 Na tena alijaribu kulitia hekalu unajisi; tukamkamata; tukataka kumhukumu kwa sheria yetu. 7 Lakini Lisia jemadari akafika akamwondoa mikononi mwetu kwa nguvu, 8 Akawaamuru wale waliomshitaki waje kwako. Wewe mwenyewe kwa kumwuliza-uliza utaweza kupata habari ya mambo yale yote tunayomshitaki sisi. 9 Wayahudi nao wakamshitaki, wakisema ya kuwa ndivyo yalivyo. 10 Na liwali alipompungia mkono ili anene, Paulo akajibu, Kwa kuwa ninajua ya kwamba wewe umekuwa mwamuzi wa taifa hili kwa muda wa miaka mingi, najitetea mwenyewe kwa moyo wa furaha. 11 Maana waweza kujua ya kuwa hazijapita siku zaidi ya kumi na mbili tangu nilipopanda kwenda Yerusalemu ili kuabudu. 12 Watu hawa hawakuniona ndani ya hekalu, nikihojiana na mtu, au kufanya fujo katika mkutano, wala katika masinagogi wala ndani ya mji. 13 Wala hawawezi kuyahakikisha mambo haya wanayonishitaki sasa. 14 Ila neno hili naungama kwako ya kwamba kwa Njia ile ambayo waiita uzushi, ndivyo ninavyomwabudu Mungu wa baba zetu, nikiyaamini yote yanayopatana na torati na yaliyoandikwa katika vyuo vya manabii. 15 Nina tumaini kwa Mungu, ambalo hata hao nao wanalitazamia, ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia. 16 Nami ninajizoeza katika neno hili niwe na dhamiri isiyo na hatia mbele za Mungu na mbele ya watu siku zote. 17 Baada ya miaka mingi nalifika niwaletee watu wa taifa langu sadaka na matoleo. 18 Wakaniona ndani ya hekalu nikishughulika na mambo haya, hali nimetakaswa, wala sikuwa na mkutano wala ghasia; lakini walikuwako baadhi ya Wayahudi waliotoka Asia, 19 ambao imewapasa hao kuwapo hapa mbele yako na kunishitaki, kama wana neno lo lote juu yangu. 20 Au watu hawa wenyewe na waseme, ni kosa gani waliloliona kwangu niliposimama mbele ya baraza, 21 isipokuwa kwa ajili ya sauti hii moja, nilipolia nikisimama katikati yao, na kusema, Kwa ajili ya ufufuo wa wafu ninahukumiwa mbele yenu hivi leo. 22 Basi Feliki aliwaahirisha, kwa sababu alijua habari za Njia ile kwa usahihi zaidi, akasema, Lisia jemadari atakapotelemka nitakata maneno yenu. 23 Akamwamuru yule akida kwamba Paulo alindwe; ila awe na nafasi, wala asimkataze mmojawapo wa rafiki zake kumtumikia. 24 Baada ya siku kadha wa kadha, Feliki akafika pamoja na Drusila mkewe aliyekuwa Myahudi, akatuma kumwita Paulo akamsikiliza habari za imani iliyo kwa Kristo Yesu. 25 Na Paulo alipokuwa akitoa hoja zake katika habari ya haki, na kuwa na kiasi, na hukumu itakayokuja, Feliki akafanya hofu akajibu, Sasa enenda zako, nami nikipata nafasi nitakuita. 26 Pamoja na hayo alitaraji kwamba atapewa fedha na Paulo; kwa hiyo alimwita mara nyingi akaongea naye. 27 Na miaka miwili ilipotimia, Feliki akampokea Porkio Festo atawale badala yake. Na Feliki, akitaka kuwafanyia Wayahudi fadhili, akamwacha Paulo amefungwa.

Matendo ya Mitume 25

1 Hata Festo alipokwisha kuingia katika uliwali, baada ya siku tatu akapanda kwenda Yerusalemu kutoka Kaisaria. 2 Kuhani Mkuu na wakuu wa Wayahudi wakampasha habari za Paulo, wakamsihi, 3 na kumwomba fadhili juu yake, kwamba atoe amri aletwe Yerusalemu, wapate kumwotea na kumwua njiani. 4 Lakini Festo akajibu ya kwamba Paulo analindwa Kaisaria; naye mwenyewe yu tayari kwenda huko karibu. 5 Akasema, Wale walio na mamlaka kwenu na watelemke pamoja nami wakamshitaki, ikiwa liko neno baya katika mtu huyu. 6 Alipokwisha kukaa kwao siku nane au kumi si zaidi, akatelemkia Kaisaria; hata siku ya pili akaketi katika kiti cha hukumu akaamuru Paulo aletwe. 7 Alipokuja, wale Wayahudi walioshuka kutoka Yerusalemu wakasimama karibu yake wakaleta mashitaka mengi mazito juu yake, wasiyoweza kuyayakinisha. 8 Paulo akasema akijitetea, Mimi sikukosa neno juu ya sheria ya Wayahudi, wala juu ya hekalu, wala juu ya Kaisari. 9 Lakini Festo akitaka kujipendekeza kwa Wayahudi akamjibu Paulo, akisema, Je! Wataka kwenda Yerusalemu, ukahukumiwe huko mbele yangu kwa ajili ya mambo hayo? 10 Paulo akasema, Mimi ninasimama hapa mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari, ndipo panipasapo kuhukumiwa; sikuwakosa Wayahudi neno, kama wewe ujuavyo sana. 11 Basi ikiwa ni mkosa au nimetenda neno la kustahili kufa, sikatai kufa; bali, kama si kweli neno hili wanalonishitaki, hapana awezaye kunitia mikononi mwao. Nataka rufani kwa Kaisari. 12 Basi Festo alipokwisha kusema na watu wa baraza, akajibu, Umetaka rufani kwa Kaisari! Basi, utakwenda kwa Kaisari. 13 Siku kadha wa kadha zilipokwisha kupita, Agripa mfalme na Bernike wakafika Kaisaria, wakimwamkia Festo. 14 Na walipokuwa wakikaa huko siku nyingi, Festo akamweleza mfalme habari za Paulo, akisema, Yupo hapa mtu mmoja aliyeachwa na Feliki kifungoni; 15 ambaye nilipokuwa Yerusalemu wakuu wa makuhani na wazee wa Wayahudi wakaniarifu habari zake, wakinitaka hukumu juu yake. 16 Nikawajibu kwamba si desturi ya Warumi kumtoa mtu awaye yote, kabla mtu yule aliyeshitakiwa hajaonana na washitaki wake uso kwa uso, na kupewa nafasi ya kujitetea katika mashitaka yake. 17 Basi walipokutanika hapa sikukawia; bali siku ya pili nikaketi katika kiti cha hukumu nikaamuru mtu huyo aletwe. 18 Na wale waliomshitaki waliposimama hawakuleta neno lo lote baya, kama nilivyodhani, 19 bali walikuwa na maswali mengine mengine juu yake katika dini yao wenyewe, na katika habari ya mtu mmoja Yesu, aliyekuwa amekwisha kufa, ambaye Paulo alikaza kusema kwamba yu hai. 20 Nami nikaona shaka jinsi ya kutafuta hakika ya habari hii, nikamwuliza kama anataka kwenda Yerusalemu ahukumiwe huko katika mambo haya. 21 Lakini Paulo alipodai kuwekwa ahukumiwe na Kaisari, nikaamuru alindwe hata nitakapompeleka kwa Kaisari. 22 Agripa akamwambia Festo, Mimi nami nalikuwa nikitaka kumsikia mtu huyu. Akasema, Utamsikia kesho. 23 Hata asubuhi Agripa akaja pamoja na Bernike kwa fahari nyingi, wakaingia mahali pa kusikia maneno, pamoja na maakida wakuu na watu wakuu wa mji; Festo akatoa amri, Paulo akaletwa. 24 Festo akasema, Mfalme Agripa, na ninyi nyote mliopo hapa pamoja nasi, mnamwona mtu huyu, ambaye jamii yote ya Wayahudi huko Yerusalemu na hapa pia wamenitaka niwasaidie, wakipiga kelele kwamba haimpasi kuishi zaidi. 25 Lakini mimi naliona kwamba hakutenda neno la kustahili kuuawa, na yeye mwenyewe alipotaka kuhukumiwa na Kaisari, nalikusudia kumpeleka kwake. 26 Nami katika habari yake sina neno la hakika la kumwandikia bwana. Kwa hiyo nimemleta hapa mbele yenu, hasa mbele yako wewe, mfalme Agripa, ili akiisha kuulizwa-ulizwa nipate neno la kuandika. 27 Kwa maana naona ni neno lisilo maana kumpeleka mfungwa, bila kuonyesha mashitaka yale aliyoshitakiwa.

Matendo ya Mitume 26

1 Agripa akamwambia Paulo, Una ruhusa kusema maneno yako. Ndipo Paulo akanyosha mkono wake, akajitetea, 2 Najiona nafsi yangu kuwa na heri, Ee mfalme Agripa, kwa kuwa nitajitetea mbele yako leo, katika mambo yale yote niliyoshitakiwa na Wayahudi. 3 Hasa kwa sababu wewe unajua sana desturi na maswali yote waliyo nayo Wayahudi; kwa sababu hiyo nakuomba unisikilize kwa uvumilivu. 4 Kwa maana Wayahudi wote wanajua maisha yangu tangu ujana, yaliyokuwa tangu mwanzo katika taifa langu huko Yerusalemu, 5 wakinijua sana tangu mwanzo, kama wakipenda kushuhudia, ya kwamba nalikuwa Farisayo kwa kuifuata madhehebu ya dini yetu iliyo sahihi kabisa. 6 Na sasa ninasimama hapa nihukumiwe kwa ajili ya tumaini la ahadi baba zetu waliyopewa na Mungu, 7 ambayo kabila zetu kumi na mbili wanataraji kuifikia, wakimwabudu Mungu kwa bidii mchana na usiku. Nami ninashitakiwa na Wayahudi kwa ajili ya tumaini hilo, Ee Mfalme. 8 Kwa nini limedhaniwa kwenu kuwa ni neno lisilosadikika, kwamba Mungu awafufua wafu? 9 Kweli, mimi mwenyewe naliona ndani ya nafsi yangu kwamba yanipasa kutenda mambo mengi yaliyopingamana na jina lake Yesu Mnazareti; 10 nami nikayafanya hayo Yerusalemu; niliwafunga wengi miongoni mwa watakatifu ndani ya magereza, nikiisha kupewa amri na wakuu wa makuhani; na walipouawa nalitoa idhini yangu. 11 Na mara nyingi katika masinagogi yote naliwaadhibu, nikawashurutisha kukufuru; nikawaonea hasira kama mwenye wazimu, nikawaudhi hata katika miji ya ugenini. 12 Basi katika kazi hiyo nilipokuwa nikienda Dameski, mwenye mamlaka na maagizo ya wakuu wa makuhani; 13 Ee Mfalme, ndipo wakati wa adhuhuri njiani naliona nuru inatoka mbinguni ipitayo mwangaza wa jua, ikinimulikia mimi, na wale waliofuatana nami pande zote. 14 Tukaanguka nchi sote, nikasikia sauti ikisema nami kwa lugha ya kiebrania, Sauli! Sauli! Mbona waniudhi? Ni vigumu kwako kuupiga mateke mchokoo. 15 Nami nikasema, Wewe u nani, Bwana? Bwana akaniambia, Mimi ni Yesu, ambaye wewe unaniudhi. 16 Lakini inuka, usimame kwa miguu yako, maana nimekutokea kwa sababu hii, nikuweke wewe uwe mtumishi na shahidi wa mambo haya uliyoyaona, na wa mambo ambayo katika hayo nitajidhihirisha kwako; 17 nikikuokoa na watu wako, na watu wa Mataifa, ambao nakutuma kwao; 18 uwafumbue macho yao, na kuwageuza waiache giza na kuielekea nuru, waziache na nguvu za Shetani na kumwelekea Mungu; kisha wapate msamaha wa dhambi zao, na urithi miongoni mwao waliotakaswa kwa imani iliyo kwangu mimi. 19 Kwa hiyo, Ee Mfalme Agripa, sikuyaasi yale maono ya mbinguni, 20 bali kwanza niliwahubiri wale wa Dameski na Yerusalemu, na katika nchi yote ya Uyahudi, na watu wa Mataifa, kwamba watubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao. 21 Kwa sababu ya hayo Wayahudi wakanikamata ndani ya hekalu wakajaribu kuniua. 22 Basi kwa kuwa nimeupata msaada utokao kwa Mungu nimesimama hata leo hivi nikiwashuhudia wadogo kwa wakubwa, wala sisemi neno ila yale ambayo manabii na Musa waliyasema, kwamba yatakuwa; 23 ya kwamba Kristo hana budi kuteswa na ya kwamba yeye kwanza kwa kufufuliwa katika wafu atatangaza habari za nuru kwa watu wake na kwa watu wa Mataifa. 24 Alipokuwa akijitetea hivi, Festo akasema kwa sauti kuu, Paulo, una wazimu, kusoma kwako kwingi kumekugeuza akili. 25 Lakini Paulo akasema, Sina wazimu, Ee Festo mtukufu, bali nanena maneno ya kweli na ya akili kamili. 26 Kwa maana mfalme anajua habari za mambo haya, nami naweza kusema naye kwa ujasiri, kwa sababu najua sana ya kuwa hapana neno moja katika hayo asilolijua; kwa maana jambo hilo halikutendeka pembeni. 27 Mfalme Agripa, je! Wawaamini manabii? Najua ya kuwa wawaamini. 28 Agripa akamwambia Paulo, Kwa maneno machache wadhani kunifanya mimi kuwa Mkristo. 29 Paulo akamjibu, Namwomba Mungu kwamba, ikiwa kwa machache au ikiwa kwa mengi, si wewe tu ila na hao wote wanaonisikia leo wawe kama mimi, isipokuwa vifungo hivi. 30 Mfalme na liwali na Bernike na wale walioketi pamoja nao wakasimama; 31 hata walipoondoka wakasemezana, wakisema, Mtu huyu hatendi neno linalostahili kifo wala kufungwa. 32 Agripa akamwambia Festo, Mtu huyo angeweza kufunguliwa, kama asingalitaka rufani kwa Kaisari.

Matendo ya Mitume 27

1 Basi ilipoamriwa tuabiri hata Italia, wakamtia Paulo na wafungwa wengine katika mikono ya akida mmoja, jina lake Yulio, wa kikosi cha Augusto. 2 Tukapanda katika merikebu ya Adramitio iliyokuwa tayari kusafiri mpaka miji ya pwani za Asia, tukatweka; Aristarko, Mmakedonia wa Thesalonike, akiwa pamoja nasi. 3 Siku ya pili tukawasili Sidoni; Yulio akamfadhili sana Paulo akampa ruhusa kwenda kwa rafiki zake, apate kutunzwa. 4 Kutoka huko tukatweka, tukasafiri chini ya Kipro ili kuukinga upepo, kwa maana pepo zilikuwa za mbisho. 5 Tulipopita bahari ya upande wa Kilikia na Pamfilia, tukafika Mira, mji wa Likia. 6 Na huko yule akida akakuta merikebu ya Iskanderia, tayari kusafiri kwenda Italia, akatupandisha humo. 7 Tukasafiri polepole kwa muda wa siku nyingi, tukafika mpaka Nido kwa shida; na kwa sababu upepo ulikuwa ukituzuia tukapita chini ya Krete, tukaikabili Salmone. 8 Tukaipita kwa shida, pwani kwa pwani, tukafika mahali paitwapo Bandari Nzuri. Karibu na hapo pana mji uitwao Lasea. 9 Na wakati mwingi ulipokwisha kupita, na safari ikiwa ina hatari sasa, kwa sababu siku za kufunga zilikuwa zimekwisha kupita, Paulo akawaonya, 10 akawaambia, Wanaume, naona kwamba safari hii itakuwa na madhara na hasara nyingi, si ya shehena na merikebu tu, ila na ya maisha yetu pia. 11 Lakini yule akida akawasikiliza nahodha na mwenye merikebu zaidi ya yale aliyoyasema Paulo. 12 Na kwa sababu bandari ile ilikuwa haifai kukaa wakati wa baridi, wengi wao wakatoa shauri la kutweka kutoka huko ili wapate kufika Foinike, kama ikiwezekana, na kukaa huko wakati wa baridi; nayo ni bandari ya Krete, inaelekea kaskazini-mashariki na kusini-mashariki. 13 Na upepo wa kusi ulipoanza kuvuma kidogo, wakidhani ya kuwa wamepata waliyoazimu kupata, wakang'oa nanga, wakasafiri karibu na Krete pwani kwa pwani. 14 Baada ya muda mchache ukavuma upepo wa nguvu wa namna ya tufani, uitwao Eurakilo, 15 merikebu iliposhikwa, na kutoweza kushindana na upepo, tukaiacha tukachukuliwa. 16 Na tukipita upesi karibu na kisiwa kidogo kiitwacho Kauda tukadiriki kuikweza mashua; lakini kwa shida. 17 Walipokwisha kuikweza wakatumia misaada, wakaikaza merikebu kwa kupitisha kamba chini yake, nao wakiogopa wasije wakakwama katika fungu liitwalo Sirti, wakatua matanga wakachukuliwa vivi hivi. 18 Na kwa maana tulikuwa tukipigwa sana na ile tufani, siku ya pili yake wakaanza kuitupa shehena baharini. 19 Siku ya tatu wakatupa vyombo vya merikebu kwa mikono yao wenyewe. 20 Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka. 21 Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao, akasema, Wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na kutokung'oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. 22 Sasa nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi mmoja miongoni mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. 23 Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami, 24 akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. 25 Basi, wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa. 26 Lakini hatuna budi kupwelewa katika kisiwa kimoja. 27 Hata usiku wa kumi na nne ulipofika, tulipokuwa tukichukuliwa huko na huko katika bahari ya Adria, kama usiku wa manane baharia wakadhani ya kuwa wanaikaribia nchi kavu. 28 Wakatupa bildi wakapata pima ishirini, wakaendelea kidogo wakatupa bildi tena, wakapata pima kumi na tano. 29 Wakachelea tusije tukapwelewa mahali penye miamba, wakatupa nanga nne za tezi, wakaomba kuche. 30 Na baharia walipotaka kukimbia na kuiacha merikebu, wakiishusha mashua baharini kana kwamba wanataka kutupa nanga za omo, 31 Paulo akawaambia akida na askari, Hawa wasipokaa ndani ya merikebu hamtaweza kuokoka. 32 Basi askari wakazikata kamba za mashua, wakaiacha ianguke. 33 Na kulipokuwa kukipambauka Paulo akawasihi wote wale chakula, akisema, Leo ni siku ya kumi na nne kungoja na kufunga, hamkula kitu cho chote. 34 Basi nawasihi mle chakula, maana itakuwa kwa wokovu wenu; kwa maana hapana hata unywele wa kichwa cha mmoja wenu utakaopotea. 35 Alipokwisha kusema hayo akatwaa mkate, akamshukuru Mungu mbele yao wote akaumega akaanza kula. 36 Ndipo wakachangamka wote, wakala chakula wenyewe. 37 Na sisi tuliokuwa ndani ya merikebu tulipata watu mia mbili na sabini na sita. 38 Walipokwisha kushiba wakaipunguza shehena ya merikebu, wakiitupa ngano baharini. 39 Kulipokucha hawakuitambua ile nchi, ila waliona hori yenye ufuo, wakashauriana kuiegesha merikebu huko, kama ikiwezekana. 40 Wakazitupilia mbali zile nanga, na kuziacha baharini, pamoja na kuzilegeza kamba za sukani, wakalitweka tanga dogo ili liushike upepo, wakauendea ule ufuo. 41 Lakini wakafikia mahali palipokutana bahari mbili, wakaiegesha merikebu, omo ikakwama ikakaa isitikiswe, bali tezi ilikuwa imefumuliwa kwa nguvu za mawimbi. 42 Shauri la askari lilikuwa kuwaua wafungwa, mtu asiogelee na kukimbia. 43 Bali akida, akitaka kumponya Paulo, akawazuia, wasifanye kama walivyokusudia, akawaamuru wale wawezao kuogelea wajitupe kwanza baharini, wafike nchi kavu; 44 nao waliosalia, hawa juu ya mbao na hawa juu ya vitu vingine vya merikebu. Na hivyo watu wote wakapata kuifikilia nchi kavu salama.

Matendo ya Mitume 28

1 Tulipokwisha kuokoka, ndipo tulipojua ya kuwa kisiwa kile chaitwa Melita. 2 Wenyeji wakatufanyia fadhili zisizokuwa za kawaida. Kwa maana waliwasha moto, wakatukaribisha sote, kwa sababu ya mvua iliyonyesha na kwa sababu ya baridi. 3 Paulo alipokuwa amekusanya mzigo wa kuni, na kuuweka motoni, nyoka akatoka kwa ajili ya ule moto akamzonga-zonga mkononi. 4 Wenyeji walipomwona yule nyoka akilewa-lewa mkononi, wakaambiana, Hakosi mtu huyu ni mwuaji; ambaye ijapokuwa ameokoka katika bahari haki haimwachi kuishi. 5 Lakini yeye akamtukusia motoni asipate madhara. 6 Wao wakadhani ya kuwa atavimba au kuanguka chini kwa kufa ghafula; na wakiisha kumwangalia sana, na kuona kwamba halimpati dhara lo lote, wakageuka, wakasema kwamba yeye ni mungu. 7 Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa, jina lake Publio; mtu huyu akatukaribisha kwa moyo wa urafiki, akatufanya wageni wake kwa muda wa siku tatu. 8 Ikawa babaake Publio alikuwa hawezi homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumpoza. 9 Yalipokwisha kutendeka hayo wengine waliokuwa na magonjwa katika kisiwa wakaja wakapozwa; 10 nao wakatuheshimu kwa heshima nyingi; basi tulipoabiri wakatupakilia vitu vile tulivyokuwa na haja navyo. 11 Baada ya miezi mitatu tukasafiri katika merikebu ya Iskanderia iliyokuwa imekaa pale kisiwani wakati wa baridi; na alama yake ni Ndugu Pacha. 12 Tukafika Sirakusa, tukakaa siku tatu. 13 Kutoka huko tukazunguka tukafikia Regio; baada ya siku moja upepo wa kusi ukavuma, na siku ya pili tukawasili Puteoli. 14 Huko tukakuta ndugu, wakatusihi tukae nao siku saba; na hivi tukafika Rumi. 15 Na kutoka huko ndugu, waliposikia habari zetu, wakaja kutulaki mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. Paulo alipowaona alimshukuru Mungu, akachangamka. 16 Tulipoingia Rumi Paulo alipewa ruhusa kukaa kwake mwenyewe pamoja na askari aliyemlinda. 17 Ikawa baada ya siku tatu akawaita wakuu wa Wayahudi wakutane, hata walipokutanika akawaambia, Ndugu zangu, ningawa sikufanya neno kinyume cha watu wetu wala neno lililopingamana na desturi za baba zetu, nalitiwa katika mikono ya Warumi, hali nimefungwa, tokea Yerusalemu. 18 Na hao walipokwisha kuniuliza-uliza walitaka kunifungua, kwa maana hapakuwa na sababu yo yote kwangu ya kuuawa. 19 Lakini Wayahudi walipotoa hoja juu ya shauri hili nalishurutishwa kutaka rufani kwa Kaisari. Si kwamba nalikuwa na neno la kuwashitaki watu wa taifa langu. 20 Basi kwa ajili ya hayo, nimewaita mje kunitazama na kusema nami; kwa maana nimefungwa kwa mnyororo huu kwa ajili ya tumaini la Israeli. 21 Wale wakamwambia, Sisi hatukupata nyaraka zenye habari zako kutoka Uyahudi, wala hapana ndugu hata mmoja aliyefika hapa na kutupasha habari, au kunena neno baya juu yako. 22 Lakini tunataka kusikia kwako uonavyo wewe; kwa maana katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali. 23 Wakiisha kuagana naye siku, wakamjia katika nyumba aliyokaa, watu wengi sana, akawaeleza kwa taratibu na kuushuhudia ufalme wa Mungu, akiwaonya mambo yake Yesu, kwa maneno ya sheria ya Musa na ya manabii, tangu asubuhi hata jioni. 24 Wengine waliamini yale yaliyonenwa, wengine hawakuyaamini. 25 Na walipokuwa hawapatani wao kwa wao, wakaenda zao, Paulo alipokwisha kusema neno hili moja, ya kwamba, Roho Mtakatifu alinena vema na baba zetu, kwa kinywa cha nabii Isaya, 26 akisema, Enenda kwa watu hawa, ukawaambie, Kusikia, mtasikia wala hamtafahamu; Na kuona, mtaona wala hamtatambua; 27 Kwa maana mioyo ya watu hawa imepumbaa, Na masikio yao ni mazito ya kusikia, Na macho yao wameyafumba; Wasije wakaona kwa macho yao, Na kusikia kwa masikio yao, Na kufahamu kwa mioyo yao, Na kubadili nia zao, nikawaponya. 28 Basi ijulikane kwenu ya kwamba wokovu huu wa Mungu umepelekwa kwa Mataifa, nao watasikia! 29 Alipokwisha kusema hayo, Wayahudi wakaenda zao, wakiulizana mengi wao kwa wao. 30 Akakaa muda wa miaka miwili mizima katika nyumba yake aliyokuwa ameipanga, akawakaribisha watu wote waliokuwa wakimwendea, 31 akihubiri habari za ufalme wa Mungu, na kuyafundisha mambo ya Bwana Yesu Kristo, kwa ujasiri mwingi, asikatazwe na mtu.

Warumi 1

1 Paulo, mtumwa wa Kristo Yesu, aliyeitwa kuwa mtume, na kutengwa aihubiri Injili ya Mungu; 2 ambayo Mungu amekwisha kuiahidi kwa kinywa cha manabii wake katika maandiko matakatifu; 3 yaani, habari za Mwanawe, aliyezaliwa katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili, 4 na kudhihirishwa kwa uweza kuwa Mwana wa Mungu, kwa jinsi ya roho ya utakatifu, kwa ufufuo wa wafu, Yesu Kristo Bwana wetu; 5 ambaye katika yeye tulipokea neema na utume ili mataifa yote wapate kujitiisha kwa imani, kwa ajili ya jina lake; 6 ambao katika hao ninyi mmekuwa wateule wa Yesu Kristo; 7 kwa wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu, walioitwa kuwa watakatifu. Neema na iwe kwenu na amani itokayo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo. 8 Kwanza namshukuru Mungu wangu katika Yesu Kristo kwa ajili yenu nyote, kwa kuwa imani yenu inahubiriwa katika dunia nzima. 9 Kwa maana Mungu, nimwabuduye kwa roho yangu katika Injili ya Mwana wake, ni shahidi wangu jinsi niwatajavyo pasipo kukoma, 10 siku zote katika sala zangu, nikiomba nije kwenu hivi karibu, Mungu akipenda kuifanikisha safari yangu. 11 Kwa maana ninatamani sana kuwaona, nipate kuwapa karama ya rohoni, ili mfanywe imara; 12 yaani, tufarijiane mimi na ninyi, kila mtu kwa imani ya mwenzake, yenu na yangu. 13 Lakini, ndugu zangu, sipendi msiwe na habari, ya kuwa mara nyingi nalikusudia kuja kwenu, nikazuiliwa hata sasa, ili nipate kuwa na matunda kwenu ninyi pia kama nilivyo nayo katika Mataifa wengine. 14 Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani, nawiwa na wenye hekima na wasio na hekima. 15 Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi. 16 Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia. 17 Kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa, Mwenye haki ataishi kwa imani. 18 Kwa maana ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu waipingao kweli kwa uovu. 19 Kwa kuwa mambo ya Mungu yanayojulikana yamekuwa dhahiri ndani yao, kwa maana Mungu aliwadhihirishia. 20 Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru; 21 kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza. 22 Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika; 23 wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo. 24 Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao. 25 Kwa maana waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba anayehimidiwa milele. Amina. 26 Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; 27 wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao. 28 Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa. 29 Wamejawa na udhalimu wa kila namna, uovu na tamaa na ubaya; wamejawa na husuda, na uuaji, na fitina, na hadaa; watu wa nia mbaya, wenye kusengenya, 30 wenye kusingizia, wenye kumchukia Mungu, wenye jeuri, wenye kutakabari, wenye majivuno, wenye kutunga mabaya, wasiowatii wazazi wao, 31 wasio na ufahamu, wenye kuvunja maagano, wasiopenda jamaa zao, wasio na rehema; 32 ambao wakijua sana hukumu ya haki ya Mungu, ya kwamba wayatendao hayo wamestahili mauti, wanatenda hayo, wala si hivyo tu, bali wanakubaliana nao wayatendao.

Warumi 2

1 Kwa hiyo, wewe mtu uwaye yote uhukumuye, huna udhuru; kwa maana katika hayo umhukumuyo mwingine wajihukumu mwenyewe kuwa na hatia; kwa maana wewe uhukumuye unafanya yale yale. 2 Nasi twajua ya kuwa hukumu ya Mungu ni ya kweli juu yao wafanyao hayo. 3 Wewe binadamu, uwahukumuye wale wafanyao hayo na kutenda yayo hayo mwenyewe, je! Wadhani ya kwamba utajiepusha na hukumu ya Mungu? 4 Au waudharau wingi wa wema wake na ustahimili wake na uvumilivu wake, usijue ya kuwa wema wa Mungu wakuvuta upate kutubu? 5 Bali kwa kadiri ya ugumu wako, na kwa moyo wako usio na toba, wajiwekea akiba ya hasira kwa siku ile ya hasira na ufunuo wa hukumu ya haki ya Mungu, 6 atakayemlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake; 7 wale ambao kwa saburi katika kutenda mema wanatafuta utukufu na heshima na kutokuharibika, watapewa uzima wa milele; 8 na wale wenye fitina, wasioitii kweli, bali wakubalio dhuluma, watapata hasira na ghadhabu; 9 dhiki na shida juu ya kila nafsi ya mwanadamu atendaye uovu, Myahudi kwanza na Myunani pia; 10 bali utukufu na heshima na amani kwa kila mtu atendaye mema, Myahudi kwanza na Myunani pia; 11 kwa maana hakuna upendeleo kwa Mungu. 12 Kwa kuwa wote waliokosa pasipo sheria watapotea pasipo sheria, na wote waliokosa, wenye sheria, watahukumiwa kwa sheria. 13 Kwa sababu sio wale waisikiao sheria walio wenye haki mbele za Mungu, bali ni wale waitendao sheria watakaohesabiwa haki. 14 Kwa maana watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. 15 Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe, yakiwashitaki au kuwatetea; 16 katika siku ile Mungu atakapozihukumu siri za wanadamu, sawasawa na injili yangu, kwa Kristo Yesu. 17 Lakini wewe, ukiwa unaitwa Myahudi na kuitegemea torati, na kujisifu katika Mungu, 18 na kuyajua mapenzi yake, na kuyakubali mambo yaliyo bora, nawe umeelimishwa katika torati, 19 na kujua hakika ya kuwa wewe mwenyewe u kiongozi wa vipofu, mwanga wao walio gizani, 20 mkufunzi wa wajinga, mwalimu wa watoto wachanga, mwenye namna ya maarifa na ya kweli katika torati; 21 basi wewe umfundishaye mwingine, je! Hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe? 22 Wewe usemaye kwamba mtu asizini, wazini mwenyewe? Wewe uchukiaye sanamu, wateka mahekalu? 23 Wewe ujisifuye katika torati, wamvunjia Mungu heshima kwa kuiasi torati? 24 Kwa maana jina la Mungu latukanwa katika Mataifa kwa ajili yenu, kama ilivyoandikwa. 25 Kwa maana kutahiriwa kwafaa kama ukiwa mtendaji wa sheria, lakini ukiwa mvunjaji wa sheria kutahiriwa kwako kumekuwa kutokutahiriwa. 26 Basi ikiwa yeye asiyetahiriwa huyashika maagizo ya torati, je! Kutokutahiriwa kwake hakutahesabiwa kuwa kutahiriwa? 27 Na yeye asiyetahiriwa kwa asili, aishikaye torati, je! Hatakuhukumu wewe, uliye na kutahiriwa, ukaihalifu torati? 28 Maana yeye si Myahudi aliye Myahudi kwa nje tu, wala tohara siyo ile ya nje tu katika mwili; 29 bali yeye ni Myahudi aliye Myahudi kwa ndani, na tohara ni ya moyo, katika roho, si katika andiko; ambaye sifa yake haitoki kwa wanadamu bali kwa Mungu.

Warumi 3

1 Basi Myahudi ana ziada gani? Na kutahiriwa kwafaa nini? 2 Kwafaa sana kwa kila njia. Kwanza kwa kuwa wamekabidhiwa mausia ya Mungu. 3 Ni nini, basi, ikiwa baadhi yao hawakuamini? Je! Kutokuamini kwao kutaubatili uaminifu wa Mungu? 4 Hasha! Mungu aonekane kuwa amini na kila mtu mwongo; kama ilivyoandikwa, Ili ujulike kuwa una haki katika maneno yako, Ukashinde uingiapo katika hukumu. 5 Lakini, ikiwa udhalimu wetu waithibitisha haki ya Mungu, tuseme nini? Je! Mungu ni dhalimu aletaye ghadhabu? (Nasema kwa jinsi ya kibinadamu.) 6 Hasha! Kwa maana hapo Mungu atawezaje kuuhukumu ulimwengu? 7 Lakini, ikiwa kweli ya Mungu imezidi kudhihirisha utukufu wake kwa sababu ya uongo wangu, mbona mimi ningali nahukumiwa kuwa ni mwenye dhambi? 8 Kwa nini tusiseme (kama tulivyosingiziwa, na kama wengine wanavyokaza kusema ya kwamba twasema hivyo), Na tufanye mabaya, ili yaje mema? Ambao kuhukumiwa kwao kuna haki. 9 Ni nini basi? Tu bora kuliko wengine? La! Hata kidogo. Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na Wayunani ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; 10 kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. 11 Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. 12 Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. 13 Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao. 14 Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu. 15 Miguu yao ina mbio kumwaga damu. 16 Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. 17 Wala njia ya amani hawakuijua. 18 Kumcha Mungu hakupo machoni pao. 19 Basi twajua ya kuwa mambo yote inenayo torati huyanena kwa hao walio chini ya torati, ili kila kinywa kifumbwe, na ulimwengu wote uwe chini ya hukumu ya Mungu; 20 kwa sababu hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki mbele zake kwa matendo ya sheria; kwa maana kutambua dhambi huja kwa njia ya sheria. 21 Lakini sasa, haki ya Mungu imedhihirika pasipo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii; 22 ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote waaminio. Maana hakuna tofauti; 23 kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; 24 wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu; 25 ambaye Mungu amekwisha kumweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake,ili aonyeshe haki yake,kwa sababu ya kuziachilia katika ustahimili wa MUNGU dhambi zote zilzotangulia kufanywa. 26 apate kuonyesha haki yake wakati huu, ili awe mwenye haki na mwenye kumhesabu haki yeye amwaminiye Yesu. 27 Ku wapi, basi, kujisifu? Kumefungiwa nje. Kwa sheria ya namna gani? Kwa sheria ya matendo? La! Bali kwa sheria ya imani. 28 Basi, twaona ya kuwa mwanadamu huhesabiwa haki kwa imani pasipo matendo ya sheria. 29 Au je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye Mungu wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia; 30 kama kwa kweli Mungu ni mmoja, atakayewahesabia haki wale waliotahiriwa katika imani, nao wale wasiotahiriwa atawahesabia haki kwa njia ya imani iyo hiyo. 31 Basi, je! Twaibatilisha sheria kwa imani hiyo? Hasha! Kinyume cha hayo twaithibitisha sheria.

Warumi 4

1 Basi, tusemeje juu ya Ibrahimu, baba yetu kwa jinsi ya mwili? 2 Kwa maana ikiwa Ibrahimu alihesabiwa haki kwa ajili ya matendo yake, analo la kujisifia; lakini si mbele za Mungu. 3 Maana maandiko yasemaje? Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa haki. 4 Lakini kwa mtu afanyaye kazi, ujira wake hauhesabiwi kuwa ni neema, bali kuwa ni deni. 5 Lakini kwa mtu asiyefanya kazi, bali anamwamini yeye ambaye amhesabia haki asiyekuwa mtauwa, imani yake mtu huyo imehesabiwa kuwa haki. 6 Kama vile Daudi aunenavyo uheri wake mtu yule ambaye Mungu amhesabia kuwa na haki pasipo matendo, 7 Heri waliosamehewa makosa yao, Na waliositiriwa dhambi zao. 8 Heri mtu yule ambaye Bwana hamhesabii dhambi. 9 Basi je! Uheri huo ni kwa hao waliotahiriwa, au kwa hao pia wasiotahiriwa? Kwa kuwa twanena ya kwamba kwake Ibrahimu imani yake ilihesabiwa kuwa ni haki. 10 Alihesabiwaje basi? Alipokwisha kutahiriwa, au kabla hajatahiriwa? Si baada ya kutahiriwa, bali kabla ya kutahiriwa. 11 Naye aliipokea dalili hii ya kutahiriwa, muhuri ya ile haki ya imani aliyokuwa nayo kabla hajatahiriwa; apate kuwa baba yao wote waaminio, ijapokuwa hawakutahiriwa, ili na wao pia wahesabiwe haki; 12 tena awe baba ya kutahiriwa, kwa wale ambao si waliotahiriwa tu, bali pia wanazifuata nyayo za imani yake baba yetu Ibrahimu aliyokuwa nayo kabla hajatahiriwa. 13 Kwa maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa imani. 14 Maana ikiwa wale wa sheria ndio warithi, imani imekuwa bure, na ahadi imebatilika. 15 Kwa sababu sheria ndiyo ifanyayo hasira; maana pasipokuwapo sheria, hapana kosa. 16 Kwa hiyo ilitoka katika imani, iwe kwa njia ya neema, ili kwamba ile ahadi iwe imara kwa wazao wote; si kwa wale wa torati tu, ila na kwa wale wa imani ya Ibrahimu; aliye baba yetu sisi sote; 17 (kama ilivyoandikwa, Nimekuweka kuwa baba wa mataifa mengi); mbele zake yeye aliyemwamini, yaani Mungu, mwenye kuwahuisha wafu, ayatajaye yale yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako. 18 Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ili apate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. 19 Yeye asiyekuwa dhaifu wa imani, alifikiri hali ya mwili wake uliokuwa umekwisha kufa, (akiwa amekwisha kupata umri wa kama miaka mia), na hali ya kufa ya tumbo lake Sara. 20 Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini, bali alitiwa nguvu kwa imani, akimtukuza Mungu; 21 huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi. 22 Kwa hiyo ilihesabiwa kwake kuwa ni haki. 23 Walakini haikuandikwa kwa ajili yake tu kwamba ilihesabiwa kwake; 24 bali na kwa ajili yetu sisi mtakaohesabiwa vivyo hivyo, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu; 25 ambaye alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili mpate kuhesabiwa haki.

Warumi 5

1 Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika imani, na mwe na amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, 2 ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo mnasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu. 3 Wala si hivyo tu, ila na mfurahi katika dhiki pia; mkijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi; 4 na kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; 5 na tumaini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi. 6 Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. 7 Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. 8 Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. 9 Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. 10 Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. 11 Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho. 12 Kwa hiyo, kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi; 13 maana kabla ya sheria dhambi ilikuwamo ulimwenguni, lakini dhambi haihesabiwi isipokuwapo sheria; 14 walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpaka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, aliye mfano wake yeye atakayekuja. 15 Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi. 16 Wala kadiri ya yule mtu mmoja aliyefanya dhambi si kadiri ya kile kipawa; kwa maana hukumu ilikuja kwa njia ya mtu mmoja ikaleta adhabu; bali karama ya neema ilikuja kwa ajili ya makosa mengi, ikaleta kuhesabiwa haki. 17 Kwa maana ikiwa kwa kukosa mtu mmoja mauti ilitawala kwa sababu ya yule mmoja, zaidi sana wao wapokeao wingi wa neema, na kile kipawa cha haki, watatawala katika uzima kwa yule mmoja, Yesu Kristo. 18 Basi tena, kama kwa kosa moja watu wote walihukumiwa adhabu, kadhalika kwa tendo moja la haki watu wote walihesabiwa haki yenye uzima. 19 Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki. 20 Lakini sheria iliingia ili kosa lile liwe kubwa sana; na dhambi ilipozidi, neema ilikuwa nyingi zaidi; 21 ili kwamba, kama vile dhambi ilivyotawala katika mauti, vivyo hivyo kwa njia ya haki neema itawale hata uzima wa milele kwa Yesu Kristo Bwana wetu.

Warumi 6

1 Tuseme nini basi? Tudumu katika dhambi ili neema izidi kuwa nyingi? 2 Hasha! Sisi tulioifia dhambi tutaishije tena katika dhambi? 3 Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake? 4 Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima. 5 Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake; 6 mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena; 7 kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi. 8 Lakini tukiwa tulikufa pamoja na Kristo, twaamini ya kuwa tutaishi pamoja naye; 9 tukijua ya kuwa Kristo akiisha kufufuka katika wafu hafi tena, wala mauti haimtawali tena. 10 Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; lakini kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu. 11 Vivyo hivyo ninyi nanyi jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi na walio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu. 12 Basi, dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti, hata mkazitii tamaa zake; 13 wala msiendelee kuvitoa viungo vyenu kuwa silaha za dhuluma kwa dhambi; bali jitoeni wenyewe kwa Mungu kama walio hai baada ya kufa, na viungo vyenu kwa Mungu kuwa silaha za haki. 14 Kwa maana dhambi haitawatawala ninyi, kwa sababu hamwi chini ya sheria, bali chini ya neema. 15 Ni nini basi? Tufanye dhambi kwa sababu hatuwi chini ya sheria bali chini ya neema? Hasha! 16 Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni utumishi wa dhambi uletao mauti, au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki. 17 Lakini Mungu na ashukuriwe, kwa maana mlikuwa watumwa wa dhambi, lakini mliitii kwa mioyo yenu ile namna ya elimu ambayo mliwekwa chini yake; 18 na mlipokwisha kuwekwa huru mbali na dhambi, mkawa watumwa wa haki. 19 Nasema kwa jinsi ya kibinadamu kwa sababu ya udhaifu wa miili yenu. Kwa kuwa kama mlivyovitoa viungo vyenu vitumiwe na uchafu na uasi mpate kuasi, vivyo hivyo sasa vitoeni viungo vyenu vitumiwe na haki mpate kutakaswa. 20 Kwa maana mlipokuwa watumwa wa dhambi, mlikuwa huru mbali na haki. 21 Ni faida gani basi mliyopata siku zile kwa mambo hayo mnayoyatahayarikia sasa? Kwa maana mwisho wa mambo hayo ni mauti. 22 Lakini sasa mkiisha kuwekwa huru, na kuwa mbali na dhambi, na kufanywa watumwa wa Mungu, mnayo faida yenu, ndiyo kutakaswa, na mwisho wake ni uzima wa milele. 23 Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.

Warumi 7

1 Ndugu zangu, hamjui (maana nasema na hao waijuao sheria) ya kuwa torati humtawala mtu wakati anapokuwa yu hai? 2 Kwa maana mwanamke aliye na mume amefungwa na sheria kwa yule mume wakati anapokuwa yu hai; bali akifa yule mume, amefunguliwa ile sheria ya mume. 3 Basi wakati awapo hai mumewe, kama akiwa na mume mwingine huitwa mzinzi. Ila mumewe akifa, amekuwa huru, hafungwi na sheria hiyo, hata yeye si mzinzi, ajapoolewa na mume mwingine. 4 Kadhalika, ndugu zangu, ninyi pia mmeifia torati, kwa njia ya mwili wa Kristo, mpate kuwa mali ya mwingine, yeye aliyefufuka katika wafu, kusudi tumzalie Mungu matunda. 5 Kwa maana tulipokuwa katika hali ya mwili, tamaa za dhambi, zilizokuwako kwa sababu ya torati, zilitenda kazi katika viungo vyetu hata mkaizalia mauti mazao. 6 Bali sasa tumefunguliwa katika torati, tumeifia hali ile iliyotupinga, ili sisi tupate kutumika katika hali mpya ya roho, si katika hali ya zamani, ya andiko. 7 Tusemeje, basi? Torati ni dhambi? Hasha! Walakini singalitambua dhambi ila kwa sheria; kwa kuwa singalijua kutamani, kama torati isingalisema, Usitamani. 8 Lakini dhambi ilipata nafasi kwa ile amri, ikafanya ndani yangu kila namna ya kutamani. Kwa maana dhambi bila sheria imekufa. 9 Nami nalikuwa hai hapo kwanza bila sheria; ila ilipokuja ile amri, dhambi ilihuika, nami nikafa. 10 Nikaona ile amri iletayo uzima ya kuwa kwangu mimi ilileta mauti. 11 Kwa maana dhambi, kwa kupata nafasi kwa ile amri, ilinidanganya, na kwa hiyo ikaniua. 12 Basi torati ni takatifu, na ile amri ni takatifu, na ya haki, na njema. 13 Basi je! Ile iliyo njema ilikuwa mauti kwangu mimi? Hasha! Bali dhambi, ili ionekane kuwa ni dhambi hasa, ilifanya mauti ndani yangu kwa njia ya ile njema, kusudi kwa ile amri dhambi izidi kuwa mbaya mno. 14 Kwa maana twajua ya kuwa torati asili yake ni ya rohoni; bali mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi. 15 Maana sijui nifanyalo, kwa sababu lile nilipendalo, silitendi; bali lile nilichukialo ndilo ninalolitenda. 16 Lakini kama nikilitenda lile nisilolipenda, naikiri ile sheria ya kuwa ni njema. 17 Basi sasa si mimi nafsi yangu ninayetenda hilo, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu 18 Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa kutaka nataka, bali kutenda lililo jema sipati. 19 Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. 20 Basi kama lile nisilolipenda ndilo nilitendalo, si mimi nafsi yangu nilitendaye, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu. 21 Basi nimeona sheria hii, ya kuwa kwangu mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya. 22 Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, 23 lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu. 24 Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? 25 Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.

Warumi 8

1 Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. 2 Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti. 3 Maana yale yasiyowezekana kwa sheria, kwa vile ilivyokuwa dhaifu kwa sababu ya mwili, Mungu, kwa kumtuma Mwanawe mwenyewe katika mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kwa sababu ya dhambi, aliihukumu dhambi katika mwili; 4 ili maagizo ya torati yatimizwe ndani yetu sisi, tusioenenda kwa kufuata mambo ya mwili, bali mambo ya roho. 5 Kwa maana wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho. 6 Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani. 7 Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuitii. 8 Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu. 9 Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake. 10 Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu i hai, kwa sababu ya haki. 11 Lakini, ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu. 12 Basi, kama ni hivyo, ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili, 13 kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. 14 Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu. 15 Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba. 16 Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; 17 na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye. 18 Kwa maana nayahesabu mateso ya wakati huu wa sasa kuwa si kitu kama utukufu ule utakaofunuliwa kwetu. 19 Kwa maana viumbe vyote pia vinatazamia kwa shauku nyingi kufunuliwa kwa wana wa Mungu. 20 Kwa maana viumbe vyote pia vilitiishwa chini ya ubatili; si kwa hiari yake, ila kwa sababu yake yeye atiyevitiisha katika tumaini; 21 kwa kuwa viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu. 22 Kwa maana twajua ya kuwa viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa. 23 Wala si hivyo tu; ila na sisi wenyewe tulio na malimbuko ya Roho, sisi pia tunaugua katika nafsi zetu, tukikutazamia kufanywa wana, yaani, ukombozi wa mwili wetu. 24 Kwa maana tuliokolewa kwa taraja; lakini kitu kilichotarajiwa kikionekana, hakuna taraja tena. Kwa maana ni nani anayekitarajia kile akionacho? 25 Bali tukikitarajia kitu tusichokiona, twakingojea kwa saburi. 26 Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. 27 Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu. 28 Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. 29 Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. 30 Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza. 31 Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? 32 Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? 33 Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. 34 Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. 35 Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? 36 Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. 37 Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. 38 Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, 39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.

Warumi 9

1 Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika Roho Mtakatifu, 2 ya kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu. 3 Kwa maana ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili; 4 ambao ni Waisraeli, wenye kule kufanywa wana, na ule utukufu, na maagano, na kupewa torati, na ibada ya Mungu, na ahadi zake; 5 ambao mababu ni wao, na katika hao alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili. Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu, mwenye kuhimidiwa milele. Amina. 6 Si kana kwamba neno la Mungu limetanguka. Maana hawawi wote Waisraeli walio wa uzao wa Israeli. 7 Wala hawawi wote wana kwa kuwa wazao wa Ibrahimu, bali, Katika Isaka wazao wako wataitwa; 8 yaani, si watoto wa mwili walio watoto wa Mungu, bali watoto wa ile ahadi wanahesabiwa kuwa wazao. 9 Kwa maana neno la ahadi ni hili, Panapo wakati huu nitakuja, na Sara atakuwa na mwana. 10 Wala si hivyo tu, lakini Rebeka naye, akiisha kuchukua mimba kwa mume mmoja, naye ni Isaka, baba yetu, 11 (kwa maana kabla hawajazaliwa wale watoto, wala hawajatenda neno jema wala baya, ili lisimame kusudi la Mungu la kuchagua, si kwa sababu ya matendo, bali kwa sababu ya nia yake aitaye), 12 aliambiwa hivi, Mkubwa atamtumikia mdogo. 13 Kama ilivyoandikwa, Nimempenda Yakobo, bali Esau nimemchukia. 14 Tuseme nini basi? Kuna udhalimu kwa Mungu? Hasha! 15 Maana amwambia Musa, Nitamrehemu yeye nimrehemuye, nitamhurumia yeye nimhurumiaye. 16 Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu. 17 Kwa maana maandiko yasema juu ya Farao, ya kwamba, Nilikusimamisha kwa kusudi hili, ili nionyeshe nguvu zangu kwako, jina langu likatangazwe katika nchi yote. 18 Basi, kama ni hivyo, atakaye kumrehemu humrehemu, na atakaye kumfanya mgumu humfanya mgumu. 19 Basi, utaniambia, Mbona angali akilaumu? Kwa maana ni nani ashindanaye na kusudi lake? 20 La! Sivyo, Ee binadamu; wewe u nani umjibuye Mungu? Je! Kitu kilichoumbwa kimwambie yeye aliyekiumba, Kwani kuniumba hivi? 21 Au mfinyanzi je! Hana amri juu ya udongo, kwa fungu moja la udongo kuumba chombo kimoja kiwe cha heshima, na kimoja kiwe hakina heshima? 22 Ni nini basi, ikiwa Mungu kwa kutaka kuonyesha ghadhabu yake, na kuudhihirisha uweza wake, kwa uvumilivu mwingi, alichukuliana na vile vyombo vya ghadhabu vilivyofanywa tayari kwa uharibifu; 23 tena, ili audhihirishe wingi wa utukufu wake katika vile vyombo vya rehema, alivyovitengeneza tangu zamani vipate utukufu; 24 ndio sisi aliotuita, si watu wa Wayahudi tu, ila na watu wa Mataifa pia? 25 Ni kama vile alivyosema katika Hosea, Nitawaita watu wangu wale wasiokuwa watu wangu, Na mpenzi wangu yeye asiyekuwa mpenzi wangu. 26 Tena itakuwa mahali pale walipoambiwa, Ninyi si watu wangu, Hapo wataitwa wana wa Mungu aliye hai. 27 Isaya naye atoa sauti yake juu ya Israeli, kusema, Hesabu ya wana wa Israeli,ijapokuwa ni kama mchanga wa bahari,ni mabaki yao tu watakaookolewa. 28 Kwa maana Bwana atalitekeleza neno lake juu ya nchi, akilimaliza na kulikata. 29 Tena kama Isaya alivyotangulia kunena, Kama Bwana wa majeshi asingalituachia uzao, Tungalikuwa kama Sodoma, tungalifananishwa na Gomora. 30 Tuseme nini, basi? Ya kwamba watu wa Mataifa, wasioifuata haki, walipata haki; lakini ni ile haki iliyo ya imani; 31 bali Israeli wakiifuata sheria ya haki hawakuifikilia ile sheria. 32 Kwa sababu gani? Kwa sababu hawakuifuata kwa njia ya imani, bali kana kwamba kwa njia ya matendo. Wakajikwaa juu ya jiwe lile likwazalo, 33 kama ilivyoandikwa, Tazama, naweka katika Sayuni jiwe likwazalo, na mwamba uangushao; Na kila amwaminiye hatatahayarika.

Warumi 10

1 Ndugu zangu, nitakayo sana moyoni mwangu, na dua yangu nimwombayo Mungu, ni kwa ajili yao, ili waokolewe. 2 Kwa maana nawashuhudia kwamba wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa. 3 Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe, hawakujitia chini ya haki ya Mungu. 4 Kwa maana Kristo ni mwisho wa sheria, ili kila aaminiye ahesabiwe haki. 5 Kwa maana Musa aliandika juu ya haki itokayo kwa sheria, ya kuwa, Mtu afanyaye hiyo ataishi kwa hiyo. 6 Bali ile haki ipatikanayo kwa imani yanena hivi, Usiseme moyoni mwako, Ni nani atakayepanda kwenda mbinguni? (Yaani, ni kumleta Kristo chini), 7 au, Ni nani atakayeshuka kwenda kuzimuni? (Yaani, ni kumleta Kristo juu, kutoka kwa wafu.) 8 Lakini yanenaje? Lile neno li karibu nawe, katika kinywa chako, na katika moyo wako; yaani, ni lile neno la imani tulihubirilo. 9 Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. 10 Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu. 11 Kwa maana andiko lanena, Kila amwaminiye hatatahayarika. 12 Kwa maana hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao; 13 kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka. 14 Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? 15 Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema! 16 Lakini si wote walioitii ile habari njema. Kwa maana Isaya asema, Bwana, ni nani aliyeziamini habari zetu? 17 Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo. 18 Lakini nasema, Je! Wao hawakusikia? Naam, wamesikia, Sauti yao imeenea duniani mwote, Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. 19 Lakini nasema, Je! Waisraeli hawakufahamu? Kwanza Musa anena, Nitawatia wivu kwa watu ambao si taifa, Kwa taifa lisilo na fahamu nitawaghadhibisha. 20 Na Isaya anao ujasiri mwingi, asema, Nalipatikana nao wasionitafuta, Nalidhihirika kwao wasioniulizia. 21 Lakini kwa Israeli asema, Mchana kutwa naliwanyoshea mikono watu wasiotii na wakaidi.

Warumi 11

1 Basi, nauliza, Je! Mungu aliwasukumia mbali watu wake? Hasha! Kwa kuwa mimi nami ni Mwisraeli, mmoja wa wazao wa Ibrahimu, mtu wa kabila ya Benyamini. 2 Mungu hakuwasukumia mbali watu wake aliowajua tokea awali. Au hamjui yale yaliyonenwa na maandiko juu ya Eliya? Jinsi anavyowashitaki Waisraeli mbele za Mungu, 3 Bwana, wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami nimesalia peke yangu, nao wananitafuta roho yangu. 4 Lakini ile jawabu ya Mungu yamwambiaje? Nimejisazia watu elfu saba wasiopiga goti mbele ya Baali. 5 Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema. 6 Lakini ikiwa ni kwa neema, haiwi kwa matendo tena, au hapo neema isingekuwa neema. 7 Imekuwaje basi? Kitu kile ambacho Israeli alikuwa akikitafuta hakukipata; lakini wale waliochaguliwa walikipata, na wengine walitiwa uzito. 8 Kama ilivyoandikwa, Mungu aliwapa roho ya usingizi, macho hata wasione, na masikio hata wasisikie, hata siku hii ya leo. 9 Na Daudi asema, Meza yao na iwe tanzi na mtego, Na kitu cha kuwakwaza, na malipo kwao; 10 Macho yao yatiwe giza ili wasione, Ukawainamishe mgongo wao siku zote. 11 Basi nasema, Je! Wamejikwaa hata waanguke kabisa? Hasha! Lakini kwa kosa lao wokovu umewafikilia Mataifa, ili wao wenyewe watiwe wivu. 12 Basi, ikiwa kosa lao limekuwa utajiri wa ulimwengu, na upungufu wao umekuwa utajiri wa Mataifa, je! Si zaidi sana utimilifu wao? 13 Lakini nasema na ninyi, mlio watu wa Mataifa. Basi, kwa kadiri nilivyo mtume wa watu wa Mataifa, naitukuza huduma iliyo yangu, 14 nipate kuwatia wivu walio damu moja na mimi na kuwaokoa baadhi yao. 15 Maana ikiwa kutupwa kwao kumeleta upatanisho kwa ulimwengu, je! Kukubaliwa kwao kutakuwa nini kama si uhai baada ya kufa? 16 Tena malimbuko yakiwa matakatifu, kadhalika na donge lote; na shina likiwa takatifu, matawi nayo kadhalika. 17 Lakini iwapo matawi mengine yamekatwa, na wewe mzeituni mwitu ulipandikizwa kati yao, ukawa mshirika wa shina la mzeituni na unono wake, 18 usijisifu juu ya matawi yale; au ikiwa wajisifu, si wewe ulichukuaye shina, bali ni shina likuchukualo wewe. 19 Basi utasema, Matawi yale yalikatwa kusudi ili nipandikizwe mimi. 20 Vema. Yalikatwa kwa kutokuamini kwao, na wewe wasimama kwa imani yako. Usijivune, bali uogope. 21 Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaachia matawi ya asili, wala hatakuachia wewe. 22 Tazama, basi, wema na ukali wa Mungu; kwa wale walioanguka, ukali, bali kwako wewe wema wa Mungu, ukikaa katika wema huo; kama sivyo, wewe nawe utakatiliwa mbali. 23 Na hao pia, wasipokaa katika kutokuamini kwao, watapandikizwa; kwa kuwa Mungu aweza kuwapandikiza tena. 24 Kwa maana ikiwa wewe ulikatwa ukatolewa katika mzeituni, ulio mzeituni mwitu kwa asili yake, kisha ukapandikizwa, kinyume cha asili, katika mzeituni ulio mwema, si zaidi sana wale walio wa asili kuweza kupandikizwa katika mzeituni wao wenyewe? 25 Kwa maana, ndugu zangu, sipendi msiijue siri hii, ili msijione kuwa wenye akili; ya kwamba kwa sehemu ugumu umewapata Israeli, mpaka utimilifu wa Mataifa uwasili. 26 Hivyo Israeli wote wataokoka; kama ilivyoandikwa, Mwokozi atakuja kutoka Sayuni; Atamtenga Yakobo na maasia yake. 27 Na hili ndilo agano langu nao, Nitakapowaondolea dhambi zao. 28 Basi kwa habari ya Injili wamekuwa adui kwa ajili yenu; bali kwa habari ya kule kuchaguliwa wamekuwa wapenzi kwa ajili ya baba zetu. 29 Kwa sababu karama za Mungu hazina majuto, wala mwito wake. 30 Kwa maana kama ninyi zamani mlivyomwasi Mungu, lakini sasa mmepata rehema kwa kuasi kwao; 31 kadhalika na hao wameasi sasa, ili kwa kupata rehema kwenu wao nao wapate rehema. 32 Maana Mungu amewafunga wote pamoja katika kuasi ili awarehemu wote. 33 Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! Hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani! 34 Maana ni nani aliyeijua nia ya Bwana? Au ni nani aliyekuwa mshauri wake? 35 Au ni nani aliyempa yeye kitu kwanza, naye atalipwa tena? 36 Kwa kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu una yeye milele. Amina.

Warumi 12

1 Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. 2 Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu. 3 Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani. 4 Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; 5 Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. 6 Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; 7 ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; 8 mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha. 9 Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. 10 Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu; 11 kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana; 12 kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; katika kusali, mkidumu; 13 kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni mkijitahidi. 14 Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani. 15 Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao. 16 Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili. 17 Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. 18 Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. 19 Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. 20 Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. 21 Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.

Warumi 13

1 Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo umeamriwa na Mungu. 2 Hivyo amwasiye mwenye mamlaka hushindana na agizo la Mungu; nao washindanao watajipatia hukumu. 3 Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi, wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema, nawe utapata sifa kwake; 4 kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. Lakini ufanyapo mabaya, ogopa; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu. 5 Kwa hiyo ni lazima kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila na kwa sababu ya dhamiri. 6 Kwa sababu hiyo tena mwalipa kodi; kwa kuwa wao ni wahudumu wa Mungu, wakidumu katika kazi iyo hiyo. 7 Wapeni wote haki zao; mtu wa kodi, kodi; mtu wa ushuru, ushuru; astahiliye hofu, hofu; astahiliye heshima, heshima. 8 Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria. 9 Maana kule kusema, Usizini, Usiue, Usiibe, Usitamani; na ikiwapo amri nyingine yo yote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako. 10 Pendo halimfanyii jirani neno baya; basi pendo ndilo utimilifu wa sheria. 11 Naam, tukiujua wakati, kwamba saa ya kuamka katika usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko tulipoanza kuamini 12 Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia, basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru. 13 Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu. 14 Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake.

Warumi 14

1 Yeye aliye dhaifu wa imani, mkaribisheni, walakini msimhukumu mawazo yake. 2 Mtu mmoja anayo imani, anakula vyote; lakini yeye aliye dhaifu hula mboga. 3 Yeye alaye asimdharau huyo asiyekula, wala yeye asiyekula asimhukumu huyo alaye; kwa maana Mungu amemkubali. 4 Wewe u nani unayemhukumu mtumishi wa mwingine? Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka. Naam, atasimamishwa, kwa kuwa Bwana aweza kumsimamisha. 5 Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku, mwingine aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe. 6 Yeye aadhimishaye siku, huiadhimisha kwa Bwana; naye alaye, hula kwa Bwana, kwa maana amshukuru Mungu; tena asiyekula, hali kwa Bwana, naye pia amshukuru Mungu. 7 Kwa sababu hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. 8 Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana. 9 Maana Kristo alikufa akawa hai tena kwa sababu hii, awamiliki waliokufa na walio hai pia. 10 Lakini wewe je! Mbona wamhukumu ndugu yako? Au wewe je! Mbona wamdharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu. 11 Kwa kuwa imeandikwa, Kama niishivyo, anena Bwana, kila goti litapigwa mbele zangu; Na kila ulimi utamkiri Mungu. 12 Basi ni hivyo, kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu. 13 Basi tusizidi kuhukumiana, bali afadhali toeni hukumu hii, mtu asitie kitu cha kumkwaza ndugu au cha kumwangusha. 14 Najua, tena nimehakikishwa sana katika Bwana Yesu, ya kuwa hakuna kitu kilicho najisi kwa asili yake, lakini kwake yeye akionaye kitu kuwa najisi, kwake huyo kitu kile ni najisi. 15 Na ndugu yako akiingia huzuni kwa sababu ya chakula, umeacha kwenda katika upendo. Kwa chakula chako usimharibu mtu yule ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake. 16 Basi, huo wema wenu usitajwe kwa ubaya. 17 Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu. 18 Kwa kuwa yeye amtumikiaye Kristo katika mambo hayo humpendeza Mungu, tena hukubaliwa na wanadamu. 19 Basi kama ni hivyo, na mfuate mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana. 20 Kwa ajili ya chakula usiiharibu kazi ya Mungu. Kweli, vyote ni safi; bali ni vibaya kwa mtu alaye na kujikwaza. 21 Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa. 22 Ile imani uliyo nayo uwe nayo nafsini mwako mbele za Mungu. Heri mtu yule asiyejihukumu nafsi yake katika neno lile analolikubali. 23 Lakini aliye na shaka, kama akila, amehukumiwa kuwa ana hatia, kwa maana hakula kwa imani. Na kila tendo lisilotoka katika imani ni dhambi.

Warumi 15

1 Basi imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu, wala haitupasi kujipendeza wenyewe. 2 Kila mtu miongoni mwetu na ampendeze jirani yake, apate wema, akajengwe. 3 Kwa maana Kristo naye hakujipendeza mwenyewe; bali kama ilivyoandikwa, Malaumu yao waliokulaumu wewe yalinipata mimi. 4 Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini. 5 Na Mungu mwenye saburi na faraja awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu; 6 ili kwa moyo mmoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo. 7 Kwa hiyo mkaribishane ninyi kwa ninyi, kama naye Kristo alivyotukaribisha, ili Mungu atukuzwe. 8 Kwa maana nasema, ya kwamba Kristo amefanyika mhudumu wa agano la kutahiriwa kwa ajili ya kweli ya Mungu, kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu; 9 tena ili Mataifa wamtukuze Mungu kwa ajili ya rehema zake; kama ilivyoandikwa, Kwa hiyo nitakushukuru kati ya Mataifa, Nami nitaliimbia jina lako. 10 Na tena anena, Furahini,Mataifa,pamoja na watu wake. 11 Na tena, Enyi Mataifa yote,msifuni Bwana; Enyi watu wote,mhimidini. 12 Na tena Isaya anena, Litakuwako shina la Yese, Naye aondokeaye kuwatawala Mataifa; Ndiye Mataifa watakayemtumaini. 13 Basi Mungu wa tumaini na awajaze ninyi furaha yote na amani katika kuamini, mpate kuzidi sana kuwa na tumaini, katika nguvu za Roho Mtakatifu. 14 Ndugu zangu, nimehakikishwa mimi mwenyewe kwa habari zenu ya kuwa ninyi nanyi mmejaa wema, mmejazwa elimu yote, tena mwaweza kuonyana. 15 Lakini nawaandikia, kwa ujasiri zaidi katika sehemu za waraka huu, kana kwamba kuwakumbusha, kwa neema ile niliyopewa na Mungu, 16 ili niwe mhudumu wa Kristo Yesu kati ya watu wa Mataifa, niifanyie Injili ya Mungu kazi ya ukuhani, kusudi Mataifa wawe sadaka yenye kibali, ikiisha kutakaswa na Roho Mtakatifu. 17 Basi, nina sababu ya kuona fahari katika Kristo Yesu mbele za Mungu. 18 Maana sitathubutu kutaja neno asilolitenda Kristo kwa kazi yangu, Mataifa wapate kutii, kwa neno au kwa tendo, 19 kwa nguvu za ishara na maajabu, katika nguvu za Roho Mtakatifu; hata ikawa tangu Yerusalemu, na kando kando yake, mpaka Iliriko nimekwisha kuihubiri Injili ya Kristo kwa utimilifu; 20 kadhalika nikijitahidi kuihubiri Injili, nisihubiri hapo ambapo jina la Kristo limekwisha kutajwa, nisije nikajenga juu ya msingi wa mtu mwingine; 21 bali kama ilivyoandikwa, Wale wasiohubiriwa habari zake wataona, Na wale wasiojasikia watafahamu. 22 Ndiyo sababu nalizuiwa mara nyingi nisije kwenu. 23 Lakini sasa, kwa kuwa sina wasaa tena pande hizi, tena tangu miaka mingi nina shauku kuja kwenu; 24 wakati wo wote nitakaosafiri kwenda Spania nitakuja kwenu. Kwa maana nataraji kuwaona ninyi katika kusafiri kwangu, na kusafirishwa nanyi, moyo wangu ushibe kwenu kidogo. 25 Ila sasa ninakwenda Yerusalemu, nikiwahudumu watakatifu; 26 maana imewapendeza watu wa Makedonia na Akaya kufanya changizo kwa ajili ya watakatifu huko Yerusalemu walio maskini. 27 Naam, imewapendeza, tena wamekuwa wadeni wao. Kwa maana ikiwa Mataifa wameyashiriki mambo yao ya roho, imewabidi kuwahudumu kwa mambo yao ya mwili. 28 Basi nikiisha kuimaliza kazi hiyo, na kuwatilia muhuri tunda hilo, nitapitia kwenu, kwenda Spania. 29 Nami najua ya kuwa nikija kwenu nitakuja kwa utimilifu wa baraka ya Kristo. 30 Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; 31 kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu; 32 nipate kufika kwenu kwa furaha, kama apendavyo Mungu, nikapate kupumzika pamoja nanyi. 33 Mungu wa amani na awe pamoja nanyi nyote. Amina.

Warumi 16

1 Namkabidhi kwenu Fibi, ndugu yetu, aliye mhudumu wa kanisa lililoko Kenkrea; 2 kwamba mmpokee katika Bwana, kama iwapasavyo watakatifu; mkamsaidie katika neno lo lote atakalohitaji kwenu; kwa sababu yeye naye amekuwa msaidizi wa watu wengi, akanisaidia mimi pia. 3 Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; 4 waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika nyumba yao. 5 Nisalimieni Epaineto, mpenzi wangu, aliye malimbuko ya Asia kwa Kristo. 6 Nisalimieni Mariamu, aliyejitaabisha sana kwa ajili yenu. 7 Nisalimieni Androniko na Yunia, jamaa zangu, waliofungwa pamoja nami, ambao ni maarufu miongoni mwa mitume; nao walikuwa katika Kristo kabla yangu. 8 Nisalimieni Ampliato, mpenzi wangu katika Bwana. 9 Nisalimieni Urbano, mtenda kazi pamoja nami katika Kristo, na Stakisi, mpenzi wangu. 10 Nisalimieni Apele, mwenye kukubaliwa katika Kristo. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Aristobulo. 11 Nisalimieni Herodioni, jamaa yangu. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Narkiso, walio katika Bwana. 12 Nisalimieni Trifaina na Trifosa, wenye bidii katika Bwana. Nisalimieni Persisi, mpenzi aliyejitahidi sana katika Bwana. 13 Nisalimieni Rufo, mteule katika Bwana, na mamaye, aliye mama yangu pia. 14 Nisalimieni Asinkrito, Flegoni, Herme, Patroba, Herma, na ndugu walio pamoja nao. 15 Nisalimieni Filologo na Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa, na watakatifu wote walio pamoja nao. 16 Salimianeni kwa busu takatifu. Makanisa yote ya Kristo yawasalimu. 17 Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao. 18 Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu. 19 Maana utii wenu umewafikilia watu wote; basi nafurahi kwa ajili yenu, lakini nataka ninyi kuwa wenye hekima katika mambo mema, na wajinga katika mambo mabaya. 20 Naye Mungu wa amani atamseta Shetani chini ya miguu yenu upesi. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi. Amina. 21 Timotheo, mtenda kazi pamoja nami, awasalimu, na Lukio, na Yasoni, na Sosipatro, jamaa zangu. 22 Mimi Tertio, niliyeandika waraka huu, nawasalimu katika Bwana. 23 Gayo, mwenyeji wangu na wa Kanisa lote pia awasalimu. Erasto, wakili wa mji, awasalimu, na Kwarto, ndugu yetu. 24 Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi nyote. Amina. 25 Sasa na atukuzwe yeye awezaye kuwafanya imara, sawasawa na injili yangu na kwa kuhubiriwa kwake Yesu Kristo, sawasawa na ufunuo wa ile siri iliyositirika tangu zamani za milele, 26 ikadhihirishwa wakati huu kwa maandiko ya manabii, ikajulikana na mataifa yote kama alivyoamuru Mungu wa milele, ili waitii Imani. 27 Ndiye Mungu mwenye hekima peke yake. Utukufu una yeye kwa Yesu Kristo, milele na milele. Amina.

1 Wakorintho 1

1 Paulo, aliyeitwa kuwa mtume wa Yesu Kristo kwa mapenzi ya Mungu, na Sosthene ndugu yetu, 2 kwa kanisa la Mungu lililoko Korintho, wale waliotakaswa katika Kristo Yesu, walioitwa wawe watakatifu, pamoja na wote wanaoliitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kila mahali, Bwana wao na wetu. 3 Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo. 4 Namshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema ya Mungu mliyopewa katika Kristo Yesu; 5 kwa kuwa katika kila jambo mlitajirika katika yeye, katika maneno yote, na maarifa yote; 6 kama ushuhuda wa Kristo ulivyothibitika kwenu; 7 hata hamkupungukiwa na karama yo yote, mkikutazamia sana kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo; 8 ambaye atawathibitisha hata mwisho, ili msilaumiwe siku ile ya Bwana wetu Yesu Kristo. 9 Mungu ni mwaminifu ambaye mliitwa na yeye mwingie katika ushirika wa Mwanawe, Yesu Kristo Bwana wetu. 10 Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja. 11 Kwa maana, ndugu zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba iko fitina kwenu. 12 Basi, maana yangu ni hii, ya kwamba kila mtu wa kwenu kusema, Mimi ni wa Paulo, na, Mimi ni wa Apolo, na, Mimi ni wa Kefa, na, Mimi ni wa Kristo. 13 Je! Kristo amegawanyika? Je! Paulo alisulibiwa kwa ajili yenu? Au je! Mlibatizwa kwa jina la Paulo? 14 Nashukuru, kwa sababu sikumbatiza mtu kwenu, ila Krispo na Gayo; 15 mtu asije akasema kwamba mlibatizwa kwa jina langu. 16 Tena naliwabatiza watu wa nyumbani mwa Stefana; zaidi ya hao, sijui kama nalimbatiza mtu ye yote mwingine. 17 Maana Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika. 18 Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. 19 Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa. 20 Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? 21 Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa. 22 Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima; 23 bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; 24 bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu. 25 Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu. 26 Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; 27 bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; 28 tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; 29 mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu. 30 Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi; 31 kusudi, kama ilivyoandikwa, Yeye aonaye fahari na aone fahari juu ya Bwana.

1 Wakorintho 2

1 Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. 2 Maana naliazimu nisijue neno lo lote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulibiwa. 3 Nami nalikuwako kwenu katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi. 4 Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, 5 ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu. 6 Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; 7 bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu; 8 ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu; 9 lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao. 10 Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu. 11 Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. 12 Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu. 13 Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. 14 Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. 15 Lakini mtu wa rohoni huyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu. 16 Maana, Ni nani aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo.

1 Wakorintho 3

1 Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. 2 Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, 3 kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu? 4 Maana hapo mtu mmoja asemapo, Mimi ni wa Paulo; na mwingine, Mimi ni wa Apolo, je! Ninyi si wanadamu? 5 Basi Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. 6 Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. 7 Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye. 8 Basi yeye apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe. 9 Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu. 10 Kwa kadiri ya neema ya Mungu niliyopewa, mimi, kama mkuu wa wajenzi mwenye hekima, naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini kila mtu na aangalie jinsi anavyojenga juu yake. 11 Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo. 12 Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. 13 Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. 14 Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. 15 Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto. 16 Hamjui ya kuwa ninyi mmekuwa hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? 17 Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi. 18 Mtu asijidanganye mwenyewe; kama mtu akijiona kuwa mwenye hekima miongoni mwenu katika dunia hii, na awe mpumbavu, ili apate kuwa mwenye hekima. 19 Maana hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu. Kwa maana imeandikwa, Yeye ndiye awanasaye wenye hekima katika hila yao. 20 Na tena, Bwana anayafahamu mawazo ya wenye hekima ya kwamba ni ya ubatili. 21 Basi, mtu ye yote na asijisifie wanadamu. Kwa maana vyote ni vyenu; 22 kwamba ni Paulo, au Apolo, au Kefa; au dunia, au uzima, au mauti; au vile vilivyopo sasa, au vile vitakavyokuwapo; vyote ni vyenu; 23 nanyi ni wa Kristo, na Kristo ni wa Mungu.

1 Wakorintho 4

1 Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu. 2 Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu. 3 Lakini, kwangu mimi, si kitu kabisa nihukumiwe na ninyi, wala kwa hukumu ya kibinadamu, wala sijihukumu hata nafsi yangu. 4 Maana sijui sababu ya kujishitaki nafsi yangu, lakini sihesabiwi haki kwa ajili hiyo; ila anihukumuye mimi ni Bwana. 5 Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo; ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu. 6 Basi ndugu, mambo hayo nimeyafanya kuwa mfano wa mimi na Apolo kwa ajili yenu, ili kwamba kwa mfano wetu mpate kujifunza kutokupita yale yaliyoandikwa; ili mmoja wenu asijivune kwa ajili ya huyu, kinyume cha mwenziwe. 7 Maana ni nani anayekupambanua na mwingine? Nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea? 8 Mmekwisha kushiba, mmekwisha kupata utajiri, mmemiliki pasipo sisi. Naam, laiti mngemiliki, ili sisi nasi tumiliki pamoja nanyi! 9 Maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu. 10 Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima. 11 Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao; 12 kisha twataabika tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili; 13 tukisingiziwa twasihi; tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote hata sasa. 14 Siyaandiki hayo ili kuwatahayarisha; bali kuwaonya kama watoto niwapendao. 15 Kwa kuwa ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili. 16 Basi, nawasihi mnifuate mimi. 17 Kwa sababu hii nimemtuma Timotheo kwenu, aliye mwanangu mpendwa, mwaminifu katika Bwana, atakayewakumbusha njia zangu zilizo katika Kristo, kama vile nifundishavyo kila mahali katika kila kanisa. 18 Basi wengine wamejivuna kana kwamba siji kwenu. 19 Lakini nitakuja kwenu upesi, nikijaliwa, nami nitafahamu, si neno lao tu waliojivuna, bali nguvu zao. 20 Maana ufalme wa Mungu hauwi katika neno, bali katika nguvu. 21 Mnataka vipi? Nije kwenu na fimbo, au nije katika upendo na roho ya upole?

1 Wakorintho 5

1 Yakini habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye. 2 Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo. 3 Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. 4 Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; 5 kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu. 6 Kujisifu kwenu si kuzuri. Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima? 7 Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; 8 basi na tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli. 9 Naliwaandikia katika waraka wangu, kwamba msichangamane na wazinzi. 10 Sisemi msichangamane kabisa na wazinzi wa dunia hii, au na wenye kutamani, au na wanyang'anyi, au na wenye kuabudu sanamu; maana hapo ingewalazimu kutoka katika dunia. 11 Lakini, mambo yalivyo, naliwaandikia kwamba msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang'anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye. 12 Maana yanihusu nini kuwahukumu wale walio nje? Ninyi hamwahukumu hao walio ndani? 13 Lakini hao walio nje Mungu atawahukumu. Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.

Wakorintho 6

1 Je! Mtu wa kwenu akiwa ana daawa juu ya mwenzake athubutu kushitaki mbele ya wasio haki, wala si mbele ya watakatifu? 2 Au hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu? Na ikiwa ulimwengu utahukumiwa na ninyi, je! Hamstahili kukata hukumu zilizo ndogo? 3 Hamjui ya kuwa mtawahukumu malaika, basi si zaidi sana mambo ya maisha haya? 4 Basi, mkiwa na mahali panapohukumiwa mambo ya maisha haya, mwawaweka kuwa waamuzi hao waliohesabiwa kuwa si kitu; katika kanisa? 5 Nasema hayo nipate kuwatahayarisha. Je! Ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake? 6 Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao wasioamini. 7 Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang'anywa mali zenu? 8 Bali kinyume cha hayo ninyi wenyewe mwadhulumu watu na kunyang'anya mali zao; naam, hata za ndugu zenu. 9 Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, 10 wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang'anyi. 11 Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu. 12 Vitu vyote ni halali kwangu, lakini si vyote vifaavyo; vitu vyote ni halali kwangu, lakini mimi sitatiwa chini ya uwezo wa kitu cho chote. 13 Vyakula ni kwa tumbo, na tumbo ni kwa vyakula; lakini Mungu atavitowesha vyote viwili, tumbo na vyakula. Lakini mwili si kwa zinaa, bali ni kwa Bwana, naye Bwana ni kwa mwili. 14 Naye Mungu alimfufua Bwana, na tena atatufufua sisi kwa uweza wake. 15 Je! Hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha! 16 Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, Wale wawili watakuwa mwili mmoja. 17 Lakini yeye aliyeungwa na Bwana ni roho moja naye. 18 Ikimbieni zinaa. Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe. 19 Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; 20 maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.

1 Wakorintho 7

1 Basi kwa habari ya mambo yale mliyoandika, ni heri mwanamume asimguse mwanamke. 2 Lakini kwa sababu ya zinaa kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe. 3 Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. 4 Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe. 5 Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu. 6 Lakini nasema hayo, kwa kutoa idhini yangu, si kwa amri. 7 Ila nipendalo ni kwamba watu wote wawe kama mimi nilivyo; walakini kila mtu ana karama yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi, na huyu hivi. 8 Lakini nawaambia wale wasiooa bado, na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo. 9 Lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe; maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa. 10 Lakini wale waliokwisha kuoana nawaagiza; wala hapo si mimi, ila Bwana; mke asiachane na mumewe; 11 lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe. 12 Lakini watu wengine nawaambia mimi, wala si Bwana, ya kwamba iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye asimwache. 13 Na mwanamke, ambaye ana mume asiyeamini, na mume huyo anakubali kukaa naye, asimwache mumewe. 14 Kwa maana yule mume asiyeamini hutakaswa katika mkewe; na yule mke asiyeamini hutakaswa katika mumewe; kama isingekuwa hivyo, watoto wenu wangekuwa si safi; bali sasa ni watakatifu. 15 Lakini yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani. 16 Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? Au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo? 17 Lakini kama Bwana alivyomgawia kila mtu, kama Mungu alivyomwita kila mtu, na aenende vivyo hivyo. Ndivyo ninavyoagiza katika makanisa yote. 18 Je! Mtu fulani ameitwa hali amekwisha kutahiriwa? Asijifanye kana kwamba hakutahiriwa. Mtu fulani ameitwa hali hajatahiriwa bado? Basi asitahiriwe. 19 Kutahiriwa si kitu, na kutokutahiriwa si kitu bali kuzihifadhi amri za Mungu. 20 Kila mtu na akae katika hali ile ile ambayo alikuwa nayo alipoitwa. 21 Je! Uliitwa u mtumwa? Usione ni vibaya lakini kama ukiweza kuwa na uhuru, afadhali kuutumia. 22 Kwa maana yeye aliyeitwa katika Bwana hali ya utumwa, ni huru wa Bwana. Vivyo hivyo yeye naye aliyeitwa hali ya uhuru, ni mtumwa wa Kristo. 23 Mlinunuliwa kwa thamani; msiwe watumwa wa wanadamu. 24 Ndugu zangu, kila mtu na akae mbele za Mungu katika hali iyo hiyo aliyoitwa nayo. 25 Kwa habari za wanawali sina amri ya Bwana, lakini natoa shauri langu, mimi niliyejaliwa kwa rehema za Bwana kuwa mwaminifu. 26 Basi, naona hili kuwa jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama alivyo. 27 Je! Umefungwa kwa mke? Usitake kufunguliwa. Umefunguliwa? Usitafute mke. 28 Lakini, kama ukioa, huna hatia; wala mwanamwali akiolewa, hana hatia; lakini watu kama hao watakuwa na dhiki katika mwili nami nataka kuwazuilia hayo. 29 Lakini, ndugu, nasema hivi, muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana; 30 na wale waliao kama hawalii; na wale wafurahio kama hawafurahi; na wale wanunuao, kama hawana kitu. 31 Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita. 32 Lakini nataka msiwe na masumbufu. Yeye asiyeoa hujishughulisha na mambo ya Bwana, ampendezeje Bwana; 33 bali yeye aliyeoa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mkewe. 34 Tena iko tofauti hii kati ya mke na mwanamwali. Yeye asiyeolewa hujishughulisha na mambo ya Bwana, apate kuwa mtakatifu mwili na roho. Lakini yeye aliyeolewa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mumewe. 35 Nasema hayo niwafaidie, si kwamba niwategee tanzi, bali kwa ajili ya vile vipendezavyo, tena mpate kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa na mambo mengine. 36 Lakini mtu awaye yote akiona ya kuwa hamtendei mwanamwali wake vipendezavyo, na ikiwa huyo amepita uzuri wa ujana wake, na ikiwapo haja, basi, afanye apendavyo, hatendi dhambi, na awaruhusu waoane. 37 Lakini yeye aliyesimama kwa uthabiti wa moyo wake, hana sharti, lakini aweza kuyatawala mapenzi yake, tena amekusudia moyoni mwake kumlinda mwanamwali wake, atatenda vema. 38 Basi, hivyo na amwozaye mwanamwali wake afanya vema; na yeye asiyemwoza atazidi kufanya vema. 39 Mwanamke hufungwa maadamu mumewe yu hai, lakini ikiwa mumewe amefariki, yu huru kuolewa na mtu ye yote amtakaye; katika Bwana tu. 40 Lakini heri yeye zaidi akikaa kama alivyo; ndivyo nionavyo mimi, nami nadhani ya kuwa mimi nami nina Roho wa Mungu.

1 Wakorintho 8

1 Na kwa habari ya vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu; Twajua ya kuwa sisi sote tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga. 2 Mtu akidhani ya kuwa anajua neno, hajui neno lo lote bado, kama impasavyo kujua. 3 Lakini mtu akimpenda Mungu, huyo amejulikana naye. 4 Basi kwa habari ya kuvila vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu; twajua ya kuwa sanamu si kitu katika ulimwengu, na ya kuwa hakuna Mungu ila mmoja tu. 5 Kwa maana ijapokuwa wako waitwao miungu, ama mbinguni ama duniani, kama vile walivyoko miungu mingi na mabwana wengi; 6 lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo. 7 Bali ujuzi huu haumo ndani ya watu wote; ila wengine kwa kuizoelea ile sanamu hata sasa hula kana kwamba ni kitu kilichotolewa sadaka kwa sanamu; na dhamiri zao, kwa kuwa dhaifu, hunajisika. 8 Lakini chakula hakituhudhurishi mbele za Mungu; maana, tusipokula hatupunguziwi kitu, wala tukila, hatuongezewi kitu. 9 Lakini angalieni huu uwezo wenu usije ukawakwaza wale walio dhaifu. 10 Kwa maana, mtu akikuona wewe uliye na ujuzi, umeketi chakulani ndani ya hekalu la sanamu, je! Dhamiri yake mtu huyo, kwa kuwa yu dhaifu, haitathibitika hata yeye naye ale vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu? 11 Na yule aliye dhaifu aangamizwa kwa ujuzi wako, naye ni ndugu ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake. 12 Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo. 13 Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.

1 Wakorintho 9

1 Je! Mimi si huru? Mimi si mtume? Mimi sikumwona Yesu Bwana wetu? Ninyi si kazi yangu katika Bwana? 2 Kwa maana ikiwa mimi si mtume kwa wengine, lakini ni mtume kwenu ninyi; kwa maana ninyi ndinyi muhuri ya utume wangu katika Bwana. 3 Hilo ndilo jawabu langu kwa wale wanaoniuliza. 4 Je! Hatuna uwezo wa kula na kunywa? 5 Hatuna uwezo kuchukua pamoja nasi mke aliye ndugu, kama wao mitume wengine, na ndugu wa Bwana, na Kefa? 6 Au je! Ni mimi peke yangu na Barnaba tusio na uwezo wa kutokufanya kazi? 7 Ni askari gani aendaye vitani wakati wo wote kwa gharama zake mwenyewe? Ni nani apandaye mizabibu asiyekula katika matunda yake? Au ni nani achungaye kundi, asiyekunywa katika maziwa ya kundi? 8 Je! Ninanena hayo kwa kibinadamu? Au torati nayo haisemi yayo hayo? 9 Kwa maana katika torati ya Musa imeandikwa, Usimfunge kinywa ng'ombe apurapo nafaka. Je! Hapo Mungu aangalia mambo ya ng'ombe? 10 Au yamkini anena hayo kwa ajili yetu? Naam, yaliandikwa kwa ajili yetu; kwa kuwa alimaye nafaka ni haki yake kulima kwa matumaini, naye apuraye nafaka ni haki yake kutumaini kupata sehemu yake. 11 Ikiwa sisi tuliwapandia ninyi vitu vya rohoni, je! Ni neno kubwa tukivuna vitu vyenu vya mwilini? 12 Ikiwa wengine wanashiriki uwezo huu juu yenu, sisi si zaidi? Lakini hatukuutumia uwezo huo; bali twayavumilia mambo yote tusije tukaizuia Habari Njema ya Kristo. 13 Hamjui ya kuwa wale wazifanyao kazi za hekaluni hula katika vitu vya hekalu, na wale waihudumiao madhabahu huwa na fungu lao katika vitu vya madhabahu? 14 Na Bwana vivyo hivyo ameamuru kwamba wale waihubirio Injili wapate riziki kwa hiyo Injili. 15 Lakini mimi sikutumia mambo hayo hata moja. Wala siyaandiki hayo ili iwe hivyo kwangu mimi; maana ni heri nife kuliko mtu awaye yote abatilishe huku kujisifu kwangu. 16 Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili! 17 Maana nikiitenda kazi hii kwa hiari yangu nina thawabu; ila ikiwa si kwa hiari yangu, nimeaminiwa uwakili. 18 Basi thawabu yangu ni nini? Ni hii, ya kuwa nihubiripo, nitaitoa Injili bila gharama, bila kutumia kwa utimilifu uwezo wangu nilio nao katika Injili. 19 Maana, ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. 20 Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate walio chini ya sheria. 21 Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria. 22 Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu. 23 Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine. 24 Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga mbio, hupiga mbio wote, lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate. 25 Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote; basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika. 26 Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; 27 bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.

1 Wakorintho 10

1 Kwa maana, ndugu zangu, sipendi mkose kufahamu ya kuwa baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari; 2 wote wakabatizwa wawe wa Musa katika wingu na katika bahari; 3 wote wakala chakula kile kile cha roho; 4 wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo. 5 Lakini wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani. 6 Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani. 7 Wala msiwe waabudu sanamu, kama wengine wao walivyokuwa; kama ilivyoandikwa, Watu waliketi kula na kunywa, kisha wakasimama wacheze. 8 Wala msifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu. 9 Wala tusimjaribu Bwana, kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka. 10 Wala msinung'unike, kama wengine wao walivyonung'unika, wakaharibiwa na mharabu. 11 Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani. 12 Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke. 13 Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili. 14 Kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu. 15 Nasema kama na watu wenye akili; lifikirini ninyi ninenalo. 16 Kikombe kile cha baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo? 17 Kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja. 18 Waangalieni hao Waisraeli walivyokuwa kwa jinsi ya mwili; wale wazilao dhabihu, je! Hawana shirika na madhabahu? 19 Basi niseme nini? Ya kwamba kile kilichotolewa sadaka kwa sanamu ni kitu? Au ya kwamba sanamu ni kitu? 20 Sivyo, lakini vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani. 21 Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani. 22 Au twamtia Bwana wivu? Je! Tuna nguvu zaidi ya yeye? 23 Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vifaavyo. Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vijengavyo. 24 Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake. 25 Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri; 26 maana, Dunia ni mali ya Bwana na vyote viijazavyo. 27 Na mtu asiyeamini akiwaalika, nanyi mnataka kwenda, kuleni kila kitu kiwekwacho mbele yenu bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri. 28 Lakini mtu akiwaambia, Kitu hiki kimetolewa kiwe sadaka, msile, kwa ajili yake yeye aliyeonyesha, na kwa ajili ya dhamiri. 29 Nasema, dhamiri, lakini si yako, bali ya yule mwingine. Maana kwa nini uhuru wangu uhukumiwe na dhamiri ya mtu mwingine? 30 Ikiwa mimi natumia sehemu yangu kwa shukrani, kwa nini nitukanwe, kwa ajili ya kitu nikishukuriacho? 31 Basi, mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu. 32 Msiwakoseshe Wayahudi wala Wayunani wala kanisa la Mungu, 33 vile vile kama mimi niwapendezavyo watu wote katika mambo yote, nisitake faida yangu mwenyewe, ila faida yao walio wengi, wapate kuokolewa.

1 Wakorintho 11

1 Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo. 2 Basi nawasifu, kwa sababu mmenikumbuka katika mambo yote, nanyi mmeyashika yale mapokeo vile vile kama nilivyowatolea. 3 Lakini nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu. 4 Kila mwanamume, asalipo, au anapohutubu, naye amefunikwa kichwa, yuaaibisha kichwa chake. 5 Bali kila mwanamke asalipo, au anapohutubu, bila kufunika kichwa, yuaaibisha kichwa chake; kwa maana ni sawasawa na yule aliyenyolewa. 6 Maana mwanamke asipofunikwa na akatwe nywele. Au ikiwa ni aibu mwanamke kukatwa nywele zake au kunyolewa, na afunikwe. 7 Kwa maana kweli haimpasi mwanamume kufunikwa kichwa, kwa sababu yeye ni mfano na utukufu wa Mungu. Lakini mwanamke ni utukufu wa mwanamume. 8 Maana mwanamume hakutoka katika mwanamke, bali mwanamke katika mwanamume. 9 Wala mwanamume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamke, bali mwanamke kwa ajili ya mwanamume. 10 Kwa hiyo imempasa mwanamke awe na dalili ya kumilikiwa kichwani, kwa ajili ya malaika. 11 Walakini si mwanamke pasipo mwanamume, wala mwanamume pasipo mwanamke, katika Bwana. 12 Maana kama mwanamke alitoka katika mwanamume, vile vile mwanamume naye huzaliwa na mwanamke; na vitu vyote asili yake hutoka kwa Mungu. Hukumuni ninyi wenyewe katika nafsi zenu. 13 Je! Inapendeza mwanamke amwombe Mungu asipofunikwa kichwa? 14 Je! Hayo maumbile yenyewe hayawafundishi ya kwamba mwanamume akiwa na nywele ndefu ni aibu kwake? 15 Lakini mwanamke akiwa na nywele ndefu ni fahari kwake. Kwa sababu amepewa zile nywele ndefu ili ziwe badala ya mavazi. 16 Lakini mtu ye yote akitaka kuleta fitina, sisi hatuna desturi kama hiyo, wala makanisa ya Mungu. 17 Lakini katika kuagiza haya, siwasifu, ya kwamba mnakusanyika, si kwa faida bali kwa hasara. 18 Kwa maana kwanza mkutanikapo kanisani nasikia kuna faraka kwenu; nami nusu nasadiki; 19 kwa maana lazima kuwapo na uzushi kwenu, ili waliokubaliwa wawe dhahiri kwenu. 20 Basi mkutanikapo pamoja haiwezekani kula chakula cha Bwana; 21 kwa maana kila mmoja hutangulia kutwaa chakula chake katika kule kula; hata huyu ana njaa, na huyu amelewa. 22 Je! Hamna nyumba za kulia na kunywea? Au mnalidharau kanisa la Mungu, na kuwatahayarisha hao wasio na kitu? Niwaambieni? Niwasifu? La! Siwasifu kwa ajili ya hayo. 23 Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, 24 naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. 25 Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. 26 Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo. 27 Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana. 28 Lakini mtu ajihoji mwenyewe, na hivyo aule mkate, na kukinywea kikombe. 29 Maana alaye na kunywa, hula na kunywa hukumu ya nafsi yake, kwa kutokuupambanua ule mwili. 30 Kwa sababu hiyo wako wengi kwenu walio hawawezi na dhaifu, na watu kadha wa kadha wamelala. 31 Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa. 32 Ila tuhukumiwapo, twarudiwa na Bwana, isije ikatupasa adhabu pamoja na dunia. 33 Kwa hiyo, ndugu zangu, mkutanikapo mpate kula, mngojaneni; 34 mtu akiwa na njaa, na ale nyumbani kwake; msipate kukutanika kwa hukumu. Na hayo yaliyosalia nijapo nitayatengeneza.

1 Wakorintho 12

1 Basi, ndugu zangu, kwa habari ya karama za roho, sitaki mkose kufahamu. 2 Mwajua ya kuwa mlipokuwa watu wa Mataifa, mlichukuliwa kufuata sanamu zisizonena, kama mlivyoongozwa. 3 Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika Roho wa Mungu, kusema, Yesu amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu. 4 Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule. 5 Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni yeye yule. 6 Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. 7 Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. 8 Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; 9 mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; 10 na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; 11 lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye. 12 Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. 13 Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja. 14 Kwa maana mwili si kiungo kimoja, bali ni vingi. 15 Mguu ukisema, Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si wa mwili; je! Si wa mwili kwa sababu hiyo? 16 Na sikio likisema, Kwa kuwa mimi si jicho, mimi si la mwili; je! Si la mwili kwa sababu hiyo? 17 Kama mwili wote ukiwa jicho, ku wapi kusikia? Kama wote ni sikio ku wapi kunusa? 18 Bali Mungu amevitia viungo kila kimoja katika mwili kama alivyotaka. 19 Lakini kama vyote vingekuwa kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi? 20 Lakini sasa viungo ni vingi, ila mwili ni mmoja. 21 Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa hakiwezi kuiambia miguu, Sina haja na ninyi. 22 Bali zaidi sana vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa vinyonge zaidi vyahitajiwa zaidi. 23 Na vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa havina heshima, viungo vile twavipa heshima zaidi; na viungo vyetu visivyo na uzuri vina uzuri zaidi sana. 24 Kwa maana viungo vyetu vilivyo na uzuri havina uhitaji; bali Mungu ameuungamanisha mwili, na kukipa heshima zaidi kile kiungo kilichopungukiwa; 25 ili kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe. 26 Na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho. 27 Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake. 28 Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha. 29 Je! Wote ni mitume? Wote ni manabii? Wote ni waalimu? Wote wanatenda miujiza? 30 Wote wana karama za kuponya wagonjwa? Wote wanena kwa lugha? Wote wafasiri? 31 Takeni sana karama zilizo kuu. Hata hivyo nawaonyesha njia iliyo bora.

1 Wakorintho 13

1 Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. 2 Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. 3 Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu. 4 Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; 5 haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; 6 haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; 7 huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote. 8 Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika. 9 Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; 10 lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika. 11 Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto. 12 Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana. 13 Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.

1 Wakorintho 14

1 Ufuateni upendo, na kutaka sana karama za rohoni, lakini zaidi kwamba mpate kuhutubu. 2 Maana yeye anenaye kwa lugha, hasemi na watu, bali husema na Mungu; maana hakuna asikiaye; lakini anena mambo ya siri katika roho yake. 3 Bali yeye ahutubuye, asema na watu maneno ya kuwajenga, na kuwafariji, na kuwatia moyo. 4 Yeye anenaye kwa lugha hujijenga nafsi yake; bali ahutubuye hulijenga kanisa. 5 Nami nataka ninyi nyote mnene kwa lugha, lakini zaidi sana mpate kuhutubu, maana yeye ahutubuye ni mkuu kuliko yeye anenaye kwa lugha, isipokuwa afasiri, ili kusudi kanisa lipate kujengwa. 6 Ila sasa, ndugu, nikija kwenu na kunena kwa lugha, nitawafaidia nini, isipokuwa nasema nanyi kwa njia ya ufunuo, au kwa njia ya elimu, au kwa njia ya hotuba, au kwa njia ya fundisho? 7 Hata vitu visivyo na uhai vitoapo sauti, ikiwa ni filimbi, ikiwa ni kinubi, visipotoa sauti zilizo na tofauti, itatambulikanaje ni wimbo gani unaopigwa kwa filimbi au kwa kinubi? 8 Kwa maana baragumu ikitoa sauti isiyojulikana, ni nani atakayejifanya tayari kwa vita? 9 Vivyo hivyo na ninyi, msipotoa kwa ulimi neno lililo dhahiri, neno lile linenwalo litajulikanaje? Maana mtakuwa mkinena hewani tu. 10 Yamkini ziko sauti za namna nyingi duniani, wala hakuna moja isiyo na maana. 11 Basi nisipoijua maana ya ile sauti nitakuwa kama mjinga kwake yeye anenaye; naye anenaye atakuwa mjinga kwangu. 12 Vivyo hivyo na ninyi, kwa kuwa mnatamani sana kuwa watu wenye karama za roho, takeni kwamba mzidi sana kuwa nazo ili kulijenga kanisa. 13 Kwa sababu hiyo yeye anenaye kwa lugha na aombe apewe kufasiri. 14 Maana nikiomba kwa lugha, roho yangu huomba, lakini akili zangu hazina matunda. 15 Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia; mtaimba kwa roho, tena nitaimba kwa akili pia. 16 Kwa maana wewe ukibariki kwa roho, yeye aketiye katika mahali pa mjinga ataitikaje, Amina, baada ya kushukuru kwako, akiwa hayajui usemayo? 17 Maana ni kweli, wewe washukuru vema, bali yule mwingine hajengwi. 18 Namshukuru Mungu ya kuwa nanena kwa lugha zaidi ya ninyi nyote; 19 lakini katika kanisa napenda kunena maneno matano kwa akili zangu, nipate kuwafundisha wengine, zaidi ya kunena maneno kumi elfu kwa lugha. 20 Ndugu zangu, msiwe watoto katika akili zenu; lakini katika uovu mgeuzwe watoto wachanga, bali katika akili zenu mkawe watu wazima. 21 Imeandikwa katika torati, Nitasema na watu hawa kwa watu wa lugha nyingine, na kwa midomo ya wageni, wala hata hivyo hawatanisikia, asema Bwana. 22 Basi, hizi lugha ni ishara, si kwao waaminio, bali kwao wasioamini lakini kuhutubu si kwa ajili yao wasioamini, bali kwa ajili yao waaminio. 23 Haya! Ikiwa kanisa lote limekusanyika pamoja, na wote wanene kwa lugha, kisha ikawa wameingia watu wajinga au wasioamini, je! Hawatasema ya kwamba mna wazimu? 24 Lakini wote wakihutubu, kisha akaingia mtu asiyeamini, au mjinga, abainishwa na wote, ahukumiwa na wote; 25 siri za moyo wake huwa wazi; na hivyo atamwabudu Mungu, akianguka kifudifudi, na kukiri ya kuwa Mungu yu kati yenu bila shaka. 26 Basi, ndugu, imekuwaje? Mkutanapo pamoja, kila mmoja ana zaburi, ana fundisho, ana ufunuo, ana lugha, ana tafsiri. Mambo yote na yatendeke kwa kusudi la kujenga. 27 Kama mtu akinena kwa lugha, wanene wawili au watatu, si zaidi, tena zamu kwa zamu, na mmoja na afasiri. 28 Lakini asipokuwapo mwenye kufasiri na anyamaze katika kanisa; aseme na nafsi yake tena na Mungu. 29 Na manabii wanene wawili, au watatu, na wengine wapambanue. 30 Lakini mwingine aliyeketi akifunuliwa neno, yule wa kwanza na anyamaze. 31 Kwa maana ninyi nyote mwaweza kuhutubu mmoja mmoja, ili wote wapate kujifunza, na wote wafarijiwe. 32 Na roho za manabii huwatii manabii. 33 Kwa maana Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani; vile vile kama ilivyo katika makanisa yote ya watakatifu. 34 Wanawake na wanyamaze katika kanisa, maana hawana ruhusa kunena bali watii, kama vile inenavyo torati nayo. 35 Nao wakitaka kujifunza neno lo lote, na wawaulize waume zao wenyewe nyumbani mwao; maana ni aibu wanawake kunena katika kanisa. 36 Au je! Neno la Mungu lilitoka kwenu? Au kuwafikia ninyi peke yenu? 37 Mtu akijiona kuwa ni nabii au mtu wa rohoni, na ayatambue hayo ninayowaandikia, ya kwamba ni maagizo ya Bwana. 38 Lakini mtu akiwa mjinga, na awe mjinga. 39 Kwa ajili ya hayo, ndugu, takeni sana kuhutubu, wala msizuie kunena kwa lugha. 40 Lakini mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.

1 Wakorintho 15

1 Basi, ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, 2 na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri isipokuwa mliamini bure. 3 Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; 4 na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; 5 na ya kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; 6 baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; 7 baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; 8 na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake. 9 Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. 10 Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami. 11 Basi, kama ni mimi, kama ni wale, ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini. 12 Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu? 13 Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka; 14 tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure. 15 Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi. 16 Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka. 17 Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu. 18 Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea. 19 Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote. 20 Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala. 21 Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu. 22 Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa. 23 Lakini kila mmoja mahali pake; limbuko ni Kristo; baadaye walio wake Kristo, atakapokuja. 24 Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu. 25 Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. 26 Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti. 27 Kwa kuwa, Alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake. Lakini atakaposema, Vyote vimetiishwa, ni dhahiri ya kuwa yeye aliyemtiishia vitu vyote hayumo. 28 Basi, vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake, ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote. 29 Au je! Wenye kubatizwa kwa ajili ya wafu watafanyaje? Kama wafu hawafufuliwi kamwe, kwa nini kubatizwa kwa ajili yao? 30 Na sisi, kwa nini tumo hatarini kila saa? 31 Naam, ndugu, kwa huku kujisifu kwangu niliko nako juu yenu katika Kristo Yesu Bwana wetu, ninakufa kila siku. 32 Ikiwa, kwa jinsi ya kibinadamu, nalipigana na hayawani wakali kule Efeso, nina faida gani? Wasipofufuliwa wafu, na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa. 33 Msidanganyike; Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema. 34 Tumieni akili kama ipasavyo, wala msitende dhambi; kwa maana wengine hawamjui Mungu. Ninanena hayo niwafedheheshe. 35 Lakini labda mtu atasema, Wafufuliwaje wafu? Nao huja kwa mwili gani? 36 Ewe mpumbavu! Uipandayo haihuiki, isipokufa; 37 nayo uipandayo, huupandi mwili ule utakaokuwa, ila chembe tupu, ikiwa ni ya ngano au nyingineyo; 38 lakini Mungu huipa mwili kama apendavyo, na kila mbegu mwili wake. 39 Nyama yote si nyama moja; ila nyingine ni ya wanadamu, nyingine ya hayawani, nyingine ya ndege, nyingine ya samaki. 40 Tena kuna miili ya mbinguni, na miili ya duniani; lakini fahari yake ile ya mbinguni ni mbali, na fahari yake ile ya duniani ni mbali. 41 Kuna fahari moja ya jua, na fahari nyingine ya mwezi, na fahari nyingine ya nyota; maana iko tofauti ya fahari hata kati ya nyota na nyota. 42 Kadhalika na kiyama ya watu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutokuharibika; 43 hupandwa katika aibu; hufufuliwa katika fahari; hupandwa katika udhaifu; hufufuliwa katika nguvu; 44 hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho. Ikiwa uko mwili wa asili, na wa roho pia uko. 45 Ndivyo ilivyoandikwa, Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha. 46 Lakini hautangulii ule wa roho, bali ule wa asili; baadaye huja ule wa roho. 47 Mtu wa kwanza atoka katika nchi, ni wa udongo. Mtu wa pili atoka mbinguni. 48 Kama alivyo yeye wa udongo, ndivyo walivyo walio wa udongo; na kama alivyo yeye wa mbinguni, ndivyo walivyo walio wa mbinguni. 49 Na kama tulivyoichukua sura yake yule wa udongo, kadhalika tutaichukua sura yake yeye aliye wa mbinguni. 50 Ndugu zangu, nisemayo ni haya, ya kuwa nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu; wala uharibifu kurithi kutokuharibika. 51 Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika, 52 kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika. 53 Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa. 54 Basi huu uharibikao utakapovaa kutokuharibika, na huu wa kufa utakapovaa kutokufa, hapo ndipo litakapokuwa lile neno lililoandikwa, Mauti imemezwa kwa kushinda. 55 Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako? 56 Uchungu wa mauti ni dhambi, na nguvu za dhambi ni torati. 57 Lakini Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo. 58 Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.

1 Wakorintho 16

1 Kwa habari ya ile changizo kwa ajili ya watakatifu, kama vile nilivyoamuru makanisa ya Galatia, nanyi fanyeni vivyo. 2 Siku ya kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake, kwa kadiri ya kufanikiwa kwake; ili kwamba michango isifanyike hapo nitakapokuja; 3 nami nitakapofika nitawatuma kwa nyaraka wale mtakaowachagua, wachukue hisani yenu mpaka Yerusalemu. 4 Na kama ikifaa niende na mimi, watasafiri pamoja nami. 5 Lakini nitakuja kwenu, nikiisha kupita kati ya Makedonia; maana napita kati ya Makedonia. 6 Labda nitakaa kwenu; naam, labda wakati wote wa baridi, mpate kunisafirisha ko kote nitakakokwenda. 7 Maana sipendi kuonana nanyi sasa, katika kupita tu, kwa sababu nataraji kukaa kwenu muda kidogo, Bwana akinijalia. 8 Lakini nitakaa Efeso hata Pentekoste; 9 kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao. 10 Lakini, Timotheo akija, angalieni akae kwenu pasipo hofu; maana anaifanya kazi ya Bwana vile vile kama mimi mwenyewe; 11 basi mtu ye yote asimdharau, lakini msafirisheni kwa amani, ili aje kwangu; maana ninamtazamia pamoja na ndugu zetu. 12 Lakini kwa habari za Apolo, ndugu yetu, nalimsihi sana aende kwenu pamoja na hao ndugu; ambaye si mapenzi yake kwenda sasa; lakini atakuja atakapopata nafasi. 13 Kesheni, simameni imara katika Imani, fanyeni kiume, mkawe hodari. 14 Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo. 15 Tena ndugu, nawasihi; (mnawajua watu wa nyumbani mwa Stefana kwamba ni malimbuko ya Akaya, nao wamejitia katika kazi ya kuwahudumu watakatifu); 16 watiini watu kama hawa, na kila mtu afanyaye kazi pamoja nao, na kujitaabisha. 17 Nami nafurahi kwa sababu ya kuja kwao Stefana na Fortunato na Akaiko; maana hawa wamenikirimia kwa wingi yale niliyopungukiwa kwenu. 18 Maana wameniburudisha roho yangu, na roho zenu pia; basi wajueni sana watu kama hao. 19 Makanisa ya Asia wawasalimu. Akila na Priska wawasalimu sana katika Bwana, pamoja na kanisa lililoko ndani ya nyumba yao. 20 Ndugu wote wawasalimu. Salimianeni kwa busu takatifu. 21 Hii ni salamu yangu Paulo kwa mkono wangu mwenyewe. 22 Mtu awaye yote asiyempenda Bwana, na awe amelaaniwa. Maran atha. 23 Neema ya Bwana Yesu na iwe pamoja nanyi. 24 Pendo langu na liwe pamoja nanyi nyote katika Kristo Yesu.

2 Wakorintho 1

1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu, na Timotheo ndugu yetu; kwa kanisa la Mungu lililoko Korintho, pamoja na watakatifu wote walioko katika nchi yote ya Akaya. 2 Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. 3 Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; 4 atufarijiye katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu. 5 Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo. 6 Lakini ikiwa sisi tu katika dhiki, ni kwa ajili ya faraja yenu na wokovu wenu; au ikiwa twafarijiwa, ni kwa ajili ya faraja yenu; ambayo hutenda kazi yake kwa kustahimili mateso yale yale tuteswayo na sisi. 7 Na tumaini letu kwa ajili yenu ni imara, tukijua ya kuwa kama vile mlivyo washiriki wa yale mateso, vivyo hivyo mmekuwa washiriki wa zile faraja. 8 Maana ndugu, hatupendi, msijue habari ya dhiki ile iliyotupata katika Asia, ya kwamba tulilemewa mno kuliko nguvu zetu, hata tukakata tamaa ya kuishi. 9 Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu, 10 aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa; 11 ninyi nanyi mkisaidiana nasi kwa ajili yetu katika kuomba, ili, kwa sababu ya ile karama tupewayo sisi kwa msaada wa watu wengi, watu wengi watoe shukrani kwa ajili yetu. 12 Kwa maana kujisifu kwetu ni huku, ushuhuda wa dhamiri yetu, ya kwamba kwa utakatifu na weupe wa moyo utokao kwa Mungu; si kwa hekima ya mwili, bali kwa neema ya Mungu; tulienenda katika dunia, na hasa kwenu ninyi. 13 Maana hatuwaandikii ninyi neno, ila yale msomayo, au kuyakiri; nami nataraji ya kuwa mtayakiri hayo hata mwisho; 14 vile vile kama mlivyotukiri kwa sehemu, ya kwamba sisi tu sababu ya kujisifu kwenu, kama ninyi mlivyo kwetu sisi, katika siku ile ya Bwana wetu Yesu. 15 Nami nikiwa na tumaini hilo nalitaka kufika kwenu hapo kwanza, ili mpate karama ya pili; 16 na kupita kwenu na kuendelea mpaka Makedonia; na tena toka Makedonia kurudi kwenu na kusafirishwa nanyi kwenda Uyahudi. 17 Basi, nilipokusudia hayo, je! Nalitumia kigeugeu? Au hayo niyakusudiayo, nayakusudia kwa jinsi ya mwili kwamba iwe hivi kwangu, kusema Ndiyo, ndiyo, na Siyo, siyo? 18 Lakini kama Mungu alivyo mwaminifu, neno letu kwenu si Ndiyo na siyo. 19 Maana Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, aliyehubiriwa katikati yenu na sisi, yaani, mimi na Silwano na Timotheo, hakuwa Ndiyo na siyo; bali katika yeye ni Ndiyo. 20 Maana ahadi zote za Mungu zilizopo katika yeye ni Ndiyo; tena kwa hiyo katika yeye ni Amin; Mungu apate kutukuzwa kwa sisi. 21 Basi Yeye atufanyaye imara pamoja nanyi katika Kristo, na kututia mafuta, ni Mungu, 22 naye ndiye aliyetutia muhuri akatupa arabuni ya Roho mioyoni mwetu. 23 Lakini mimi namwita Mungu awe shahidi juu ya roho yangu, ya kwamba, kwa kuwahurumia sijafika Korintho. 24 Si kwamba tunatawala imani yenu; bali tu wasaidizi wa furaha yenu; maana kwa imani yenu mnasimama.

2 Wakorintho 2

1 Lakini nafsini mwangu nalikusudia hivi, nisije kwenu tena kwa huzuni. 2 Maana mimi nikiwatia huzuni, basi ni nani anifurahishaye mimi ila yeye ahuzunishwaye nami? 3 Nami naliwaandikia neno lilo hilo, ili nijapo nisitiwe huzuni na wale ambao ilinipasa kuwafurahia; nikiwatumaini ninyi nyote kwamba furaha yangu ni yenu nyote pia. 4 Maana katika dhiki nyingi na taabu ya moyo niliwaandikia na machozi mengi; si kwamba mhuzunishwe, bali mpate kujua upendo wangu nilio nao kwenu jinsi ulivyo mwingi. 5 Lakini iwapo mtu amehuzunisha, hakunihuzunisha mimi tu, bali kwa sehemu (nisije nikalemea mno), amewahuzunisha ninyi nyote. 6 Yamtosha mtu wa namna hii adhabu ile aliyopewa na walio wengi; 7 hata kinyume cha hayo, ni afadhali mmsamehe na kumfariji, mtu kama huyo asije akamezwa katika huzuni yake ipitayo kiasi. 8 Kwa hiyo nawasihi kumthibitishia upendo wenu. 9 Maana naliandika kwa sababu hii pia, ili nipate bayana kwenu kwamba mmekuwa wenye kutii katika mambo yote. 10 Lakini kama mkimsamehe mtu neno lo lote, nami nimemsamehe; kwa maana mimi nami, ikiwa nimemsamehe mtu neno lo lote, nimemsamehe kwa ajili yenu mbele za Kristo, 11 Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake. 12 Basi nilipofika Troa kwa ajili ya Injili ya Kristo, nikafunguliwa mlango katika Bwana, 13 sikuona raha nafsini mwangu, kwa sababu sikumwona Tito ndugu yangu, bali niliagana nao, nikaondoka kwenda Makedonia. 14 Ila Mungu ashukuriwe, anayetushangiliza daima katika Kristo, na kuidhihirisha harufu ya kumjua yeye kila mahali kwa kazi yetu. 15 Kwa maana sisi tu manukato ya Kristo, mbele za Mungu, katika wao wanaookolewa, na katika wao wanaopotea; 16 katika hao wa pili harufu ya mauti iletayo mauti; katika hao wa kwanza harufu ya uzima iletayo uzima. Naye ni nani atoshaye kwa mambo hayo? 17 Kwa maana sisi si kama walio wengi, walighoshio neno la Mungu; bali kama kwa weupe wa moyo, kama kutoka kwa Mungu, mbele za Mungu, twanena katika Kristo.

2 Wakorintho 3

1 Je! Tunaanza tena kujisifu wenyewe? Au tunahitaji, kama wengine, barua zenye sifa kuja kwenu, au kutoka kwenu? 2 Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; 3 mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama. 4 Na tumaini hilo tunalo mbele za Mungu kwa njia ya Kristo. 5 Si kwamba twatosha sisi wenyewe kufikiri neno lo lote kwamba ni letu wenyewe, bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu. 6 Naye ndiye aliyetutosheleza kuwa wahudumu wa agano jipya; si wa andiko, bali wa roho; kwa maana andiko huua, bali roho huhuisha. 7 Basi, ikiwa huduma ya mauti, iliyoandikwa na kuchorwa katika mawe, ilikuja katika utukufu, hata Waisraeli hawakuweza kuukazia macho uso wa Musa, kwa sababu ya utukufu wa uso wake; nao ni utukufu uliokuwa ukibatilika; 8 je! Huduma ya roho haitazidi kuwa katika utukufu? 9 Kwa maana ikiwa huduma ya adhabu ina utukufu, siuze huduma ya haki ina utukufu unaozidi. 10 Maana hata ile iliyotukuzwa haikuwa na utukufu hivi, kwa sababu ya utukufu uzidio sana. 11 Kwa maana, ikiwa ile inayobatilika ilikuwa na utukufu, zaidi sana ile ikaayo ina utukufu. 12 Basi, kwa kuwa mna taraja la namna hii, twatumia ujasiri mwingi; 13 nasi si kama Musa alivyotia utaji juu ya uso wake, ili kwamba Waisraeli wasitazame sana mwisho wa ile iliyokuwa ikibatilika; 14 ila fikira zao zilitiwa uzito. Kwa maana hata leo hivi, wakati lisomwapo Agano la Kale, utaji uo huo wakaa; yaani, haikufunuliwa kwamba huondolewa katika Kristo; 15 ila hata leo, torati ya Musa isomwapo, utaji huikalia mioyo yao. 16 Lakini wakati wo wote watakapomgeukia Bwana, ule utaji huondolewa. 17 Basi ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru. 18 Lakini sisi sote, kwa uso usiotiwa utaji, tukiurudisha utukufu wa Bwana, kama vile katika kioo, tunabadilishwa tufanane na mfano uo huo, toka utukufu hata utukufu, kama vile kwa utukufu utokao kwa Bwana, aliye Roho.

2 Wakorintho 4

1 Kwa sababu hiyo, kwa kuwa tuna huduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei; 2 lakini tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika, wala hatuenendi kwa hila, wala kulichanganya neno la Mungu na uongo; bali kwa kuidhihirisha iliyo kweli twajionyesha kuwa na haki, dhamiri za watu zikitushuhudia mbele za Mungu. 3 Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; 4 ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu. 5 Kwa maana hatujihubiri wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi wenu kwa ajili ya Yesu. 6 Kwa kuwa Mungu, aliyesema, Nuru itang'aa toka gizani, ndiye aliyeng'aa mioyoni mwetu, atupe nuru ya elimu ya utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo. 7 Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu. 8 Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; 9 twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; 10 siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu. 11 Kwa maana sisi tulio hai, siku zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu ipatikanayo na mauti. 12 Basi hapo mauti hufanya kazi ndani yetu, bali uzima ndani yenu. 13 Lakini kwa kuwa tuna roho ile ile ya imani; kama ilivyoandikwa, Naliamini, na kwa sababu hiyo nalinena; sisi nasi twaamini, na kwa sababu hiyo twanena; 14 tukijua ya kwamba yeye aliyemfufua Bwana Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha pamoja nanyi. 15 Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe. 16 Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. 17 Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; 18 tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.

2 Wakorintho 5

1 Kwa maana twajua ya kuwa nyumba ya maskani yetu iliyo ya dunia hii ikiharibiwa, tunalo jengo litokalo kwa Mungu, nyumba isiyofanywa kwa mikono, iliyo ya milele mbinguni. 2 Maana katika nyumba hii twaugua, tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni; 3 ikiwa tukiisha kuvikwa hatutaonekana tu uchi. 4 Kwa sababu sisi tulio katika maskani hii twaugua, tukilemewa; si kwamba twataka kuvuliwa, bali kuvikwa, ili kitu kile kipatikanacho na mauti kimezwe na uzima. 5 Basi yeye aliyetufanya kwa ajili ya neno lilo hilo ni Mungu, aliyetupa arabuni ya Roho. 6 Basi siku zote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. 7 (Maana twaenenda kwa imani, si kwa kuona.) 8 Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana. 9 Kwa hiyo, tena, ikiwa tupo hapa, au ikiwa hatupo hapa, twajitahidi kumpendeza yeye. 10 Kwa maana imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya. 11 Basi tukiijua hofu ya Bwana, twawavuta wanadamu; lakini tumedhihirishwa mbele za Mungu. Nami natumaini ya kuwa tumedhihirishwa katika dhamiri zenu pia. 12 Maana hatujisifu wenyewe mbele yenu tena, bali tunawapa sababu ya kujisifu kwa ajili yetu, ili mpate kuwa nayo mbele yao wanaojisifu kwa mambo ya nje tu, wala si kwa mambo ya moyoni. 13 Maana ikiwa tumerukwa na akili zetu, ni kwa ajili ya Mungu; au ikiwa tunazo akili zetu timamu, ni kwa ajili yenu. 14 Maana, upendo wa Kristo watubidisha; maana tumehukumu hivi, ya kwamba mmoja alikufa kwa ajili ya wote, basi walikufa wote; 15 tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao. 16 Hata imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena. 17 Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya. 18 Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho; 19 yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho. 20 Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu. 21 Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye.

2 Wakorintho 6

1 Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure. 2 (Kwa maana asema, Wakati uliokubalika nalikusikia, Siku ya wokovu nalikusaidia;tazama,wakati uliokubalika ndiyo sasa; tazama siku ya wokovu ni sasa) 3 Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; 4 bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; katika saburi nyingi, katika dhiki, katika misiba, katika shida; 5 katika mapigo, katika vifungo, katika fitina, katika taabu, katika kukesha, katika kufunga; 6 katika kuwa safi, katika elimu, katika uvumilivu, katika utu wema, katika Roho Mtakatifu, katika upendo usio unafiki; 7 katika neno la kweli, katika nguvu ya Mungu; kwa silaha za haki za mkono wa kuume na za mkono wa kushoto; 8 kwa utukufu na aibu; kwa kunenwa vibaya na kunenwa vema; kama wadanganyao, bali tu watu wa kweli; 9 kama wasiojulikana, bali wajulikanao sana; kama wanaokufa, kumbe tu hai; kama wanaorudiwa, bali wasiouawa; 10 kama wenye huzuni, bali siku zote tu wenye furaha; kama maskini, bali tukitajirisha wengi; kama wasio na kitu, bali tu wenye vitu vyote. 11 Vinywa vyetu vimefumbuliwa kwenu, enyi Wakorintho; mioyo yetu imekunjuliwa. 12 Hamsongwi ndani yetu, bali mwasongwa katika mioyo yenu. 13 Basi, ili mlipe kadiri ile mliyopewa (nasema nanyi kama na watoto), nanyi pia mkunjuliwe mioyo. 14 Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? 15 Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? 16 Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. 17 Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. 18 Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,

2 Wakorintho 7

1 Basi, wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu. 2 Tupeni nafasi mioyoni mwenu. Hatukumdhulumu mtu ye yote, wala kumharibu mtu, wala kumkaramkia mtu. 3 Sisemi neno hilo ili niwahukumu ninyi kuwa na hatia; kwa maana nimetangulia kusema, ya kwamba ninyi mmo mioyoni mwetu hata kwa kufa pamoja, na kuishi pamoja. 4 Ninao ujasiri mwingi kwenu; naona fahari kuu juu yenu. Nimejaa faraja, katika dhiki yetu yote nimejaa furaha ya kupita kiasi. 5 Kwa maana hata tulipokuwa tumefika Makedonia miili yetu haikupata nafuu; bali tulidhikika kote kote; nje palikuwa na vita, ndani hofu. 6 Lakini Mungu, mwenye kuwafariji wanyonge, alitufariji kwa kuja kwake Tito. 7 Wala si kwa kuja kwake tu, bali kwa zile faraja nazo alizofarijiwa kwenu, akituarifu habari ya shauku yenu, na maombolezo yenu, na bidii yenu kwa ajili yangu, hata nikazidi kufurahi. 8 Kwa sababu, ijapokuwa naliwahuzunisha kwa waraka ule, sijuti; hata ikiwa nalijuta, naona ya kwamba waraka ule uliwahuzunisha, ingawa ni kwa kitambo tu. 9 Sasa nafurahi, si kwa sababu ya ninyi kuhuzunishwa, bali kwa sababu mlihuzunishwa, hata mkatubu. Maana mlihuzunishwa kwa jinsi ya Mungu, ili msipate hasara kwa tendo letu katika neno lo lote. 10 Maana huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu hufanya toba liletalo wokovu lisilo na majuto; bali huzuni ya dunia hufanya mauti. 11 Maana, angalieni, kuhuzunishwa kuko huko kwa jinsi ya Mungu kulitenda bidii kama nini ndani yenu; naam, na kujitetea, naam, na kukasirika, naam, na hofu, naam, na shauku, naam, na kujitahidi, naam, na kisasi! Kwa kila njia mmejionyesha wenyewe kuwa safi katika jambo hilo. 12 Basi, ijapokuwa naliwaandikia, sikuandika kwa ajili yake yeye aliyedhulumu, wala si kwa ajili yake yeye aliyedhulumiwa, bali bidii yenu kwa ajili yetu ipate kudhihirishwa kwenu mbele za Mungu. 13 Kwa hiyo tulifarijiwa. Tena katika kufarijiwa kwetu tulifurahi sana kupita kiasi kwa sababu ya furaha ya Tito; maana roho yake imeburudishwa na ninyi nyote. 14 Kwa maana, ikiwa nimejisifu mbele yake katika neno lo lote kwa ajili yenu, sikutahayarishwa; bali, kama tulivyowaambia mambo yote kwa kweli, vivyo hivyo na kujisifu kwetu kwa Tito kulikuwa kweli. 15 Na mapenzi yake kwenu yamekuwa mengi kupita kiasi, akumbukapo kutii kwenu ninyi nyote, jinsi mlivyomkaribisha kwa hofu na kutetemeka. 16 Nafurahi, kwa sababu katika kila neno nina moyo mkuu kwa ajili yenu.

2 Wakorintho 8

1 Tena ndugu zetu, twawaarifu habari ya neema ya Mungu, waliyopewa makanisa ya Makedonia; 2 maana walipokuwa wakijaribiwa kwa dhiki nyingi, wingi wa furaha yao na umaskini wao uliokuwa mwingi uliwaongezea utajiri wa ukarimu wao. 3 Maana nawashuhudia kwamba, kwa uwezo wao, na zaidi ya uwezo wao, kwa hiari yao wenyewe walitoa vitu vyao; 4 wakituomba sana pamoja na kutusihi kwa habari ya neema hii, na shirika hili la kuwahudumia watakatifu. 5 Tena walitenda hivi si kama tulivyotumaini tu, bali kwanza walijitoa nafsi zao kwa Bwana; na kwetu pia, kwa mapenzi ya Mungu. 6 Hata tukamwonya Tito kuwatimilizia neema hii kwenu kama vile yeye alivyotangulia kuianzisha. 7 Lakini kama mlivyo na wingi wa mambo yote; imani, na usemi, na elimu, na bidii yote, na upendo wenu kwetu sisi; basi vivyo hivyo mpate wingi wa neema hii pia. 8 Sineni ili kuwaamuru, bali kwa bidii ya watu wengine nijaribu unyofu wa upendo wenu. 9 Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake. 10 Nami katika neno hili natoa shauri langu; maana neno hili lawafaa ninyi mliotangulia, yapata mwaka, licha ya kutenda hata na kutaka pia. 11 Lakini sasa timizeni kule kutenda nako, ili kama vile mlivyokuwa tayari kutaka, vivyo hivyo mkawe tayari na kutimiza, kwa kadiri ya mlivyo navyo. 12 Maana, kama nia ipo, hukubaliwa kwa kadiri ya alivyo navyo mtu, si kwa kadiri ya asivyo navyo. 13 Maana sisemi hayo, ili wengine wapate raha nanyi mpate dhiki; 14 bali mambo yawe sawasawa; wakati huu wa sasa wingi wenu uwafae upungufu wao, ili na wingi wao uwafae ninyi mtakapopungukiwa; ili mambo yawe sawasawa. 15 Kama ilivyoandikwa, Aliyekusanya vingi, hakuzidi, wala yeye aliyekusanya vichache hakupungukiwa. 16 Lakini ahimidiwe Mungu atiaye bidii ile ile kwa ajili yenu katika moyo wa Tito. 17 Maana aliyapokea kweli yale maonyo; tena, huku akizidi kuwa na bidii, alisafiri kwenda kwenu kwa hiari yake mwenyewe. 18 Na pamoja naye tukamtuma ndugu yule ambaye sifa zake katika Injili zimeenea makanisani mwote. 19 Wala si hivyo tu, bali alichaguliwa na makanisa asafiri pamoja nasi katika jambo la neema hii, tunayoitumikia, ili Bwana atukuzwe, ukadhihirike utayari wetu. 20 Tukijiepusha na neno hili, mtu asije akatulaumu kwa habari ya karama hii tunayoitumikia; 21 tukitangulia kufikiri yaliyo mema, si mbele za Bwana tu, ila na mbele ya wanadamu. 22 Nasi pamoja nao tumemtuma ndugu yetu tuliyemwona mara nyingi katika mambo mengi kuwa ana bidii, na sasa ana bidii zaidi sana kwa sababu ya tumaini kuu alilo nalo kwenu. 23 Basi mtu akitaka habari za Tito, yeye ni mshirika wangu, na mtenda kazi pamoja nami kwa ajili yenu; tena akitaka habari za ndugu zetu, wao ni mitume wa makanisa, na utukufu wa Kristo. 24 Basi waonyesheni mbele ya makanisa hakika ya upendo wenu, na ya kujisifu kwetu kwa ajili yenu.

2 Wakorintho 9

1 Kwa habari za kuwahudumia watakatifu sina haja ya kuwaandikia. 2 Maana najua utayari wenu, ninaojisifia kwa ajili yenu kwa Wamakedonia, kwamba Akaya ilikuwa tayari tangu mwaka mzima; na bidii yenu imewatia moyo wengi wao. 3 Lakini naliwatuma hao ndugu, ili kujisifu kwetu kwa ajili yenu kusibatilike katika jambo hili; mpate kuwa tayari, kama nilivyosema; 4 kusudi, wakija Wamakedonia pamoja nami, na kuwakuta hamjawa tayari, tusije tukatahayarika sisi, (tusiseme ninyi), katika hali hiyo ya kutumaini. 5 Basi naliona ya kuwa ni lazima niwaonye ndugu hawa watangulie kufika kwenu, na kutengeneza mapema karama yenu mliyoahidi tangu zamani, ili iwe tayari, na hivi iwe kama kipawa, wala si kama kitu kitolewacho kwa unyimivu. 6 Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. 7 Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. 8 Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna siku zote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema; 9 kama ilivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, Haki yake yakaa milele. 10 Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye atayaongeza mazao ya haki yenu; 11 mkitajirishwa katika vitu vyote mpate kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu. 12 Maana utumishi wa huduma hii hauwatimizii watakatifu riziki walizopungukiwa tu, bali huzidi sana kuwa na faida kwa shukrani nyingi apewazo Mungu; 13 kwa kuwa mkijaribiwa kwa utumishi huo, wanamtukuza Mungu kwa ajili ya utii wenu katika kuikiri Injili ya Kristo, na kwa ajili ya ukarimu wenu mliowashirikisha wao na watu wote. 14 Nao wenyewe, wakiomba dua kwa ajili yenu, wawaonea shauku kwa sababu ya neema ya Mungu iliyozidi sana ndani yenu. 15 Mungu ashukuriwe kwa sababu ya kipawa chake, tusichoweza kukisifu kama ipasavyo.

2 Wakorintho 10

1 Basi, mimi Paulo mwenyewe nawasihi kwa upole na utaratibu wa Kristo; mimi niliye mnyenyekevu nikiwapo pamoja nanyi, bali nisipokuwapo ni mwenye ujasiri kwenu; 2 naam, naomba kwamba nikiwapo, nisiwe na ujasiri kwa uthabiti ambao nahesabu kuwa nao juu ya wale wanaodhania ya kuwa sisi tunaenenda kwa jinsi ya mwili. 3 Maana ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; 4 (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;) 5 tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo; 6 tena tukiwa tayari kupatiliza maasi yote, kutii kwenu kutakapotimia. 7 Yaangalieni yaliyo mbele ya macho yenu. Mtu akijitumainia mwenyewe ya kuwa ni mtu wa Kristo, na afikiri hivi pia nafsini mwake, ya kwamba kama yeye alivyo mtu wa Kristo, vivyo hivyo na sisi. 8 Maana, nijapojisifu zaidi kidogo kwa ajili ya mamlaka yetu, (tuliyopewa na Bwana, tupate kuwajenga wala si kuwaangusha), sitatahayarika; 9 nisije nikaonekana kana kwamba nataka kuwaogofya kwa nyaraka zangu. 10 Maana wasema, Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake si kitu. 11 Mtu kama huyo na afikiri hivi, ya kwamba jinsi tulivyo kwa maneno katika nyaraka tusipokuwapo, ndivyo tulivyo kwa matendo tukiwapo. 12 Kwa kuwa hatuthubutu kujihesabu pamoja na baadhi yao wanaojisifu wenyewe, wala kujilinganisha nao; bali wao wenyewe wakijipima nafsi zao na nafsi zao, na wakijilinganisha nafsi zao na nafsi zao, hawana akili. 13 Lakini sisi hatutajisifu zaidi ya kadiri yetu; bali kwa kadiri ya kipimo tulichopimiwa na Mungu, yaani, kadiri ya kufika hata kwenu. 14 Maana hatujitanui nafsi zetu kupita kadiri yetu, kana kwamba hatuwafikii ninyi; kwa sababu tulitangulia kufika mpaka kwenu katika injili ya Kristo; 15 wala hatujisifu zaidi ya kadiri yetu, yaani, katika taabu za watu wengine; bali tukiwa na tumaini ya kwamba, imani yenu ikuapo, tutakuzwa kwenu kwa kadiri ya kipimo chetu, na kupata ziada; 16 hata kuihubiri Injili katika nchi zilizo mbele kupita nchi zenu; tusijisifu katika kipimo cha mtu mwingine kwa mambo yaliyokwisha kutengenezwa. 17 Lakini, Yeye ajisifuye, na ajisifu katika Bwana. 18 Maana mtu mwenye kukubaliwa si yeye ajisifuye, bali yeye asifiwaye na Bwana.

2 Wakorintho 11

1 Laiti mngechukuliana nami katika upumbavu wangu kidogo! Naam, mchukuliane nami. 2 Maana nawaonea wivu, wivu wa Mungu; kwa kuwa naliwaposea mume mmoja, ili nimletee Kristo bikira safi. 3 Lakini nachelea; kama yule nyoka alivyomdanganya Hawa kwa hila yake, asije akawaharibu fikira zenu, mkauacha unyofu na usafi kwa Kristo. 4 Maana yeye ajaye akihubiri Yesu mwingine ambaye sisi hatukumhubiri, au mkipokea roho nyingine msiyoipokea, au injili nyingine msiyoikubali, mnatenda vema kuvumiliana naye! 5 Maana nadhani ya kuwa mimi sikupungukiwa na kitu walicho nacho mitume walio wakuu. 6 Lakini nijapokuwa mimi ni mtu asiyejua kunena, hii si hali yangu katika elimu; ila katika kila neno tumedhihirishwa kwenu. 7 Je! Nalifanya dhambi kwa kunyenyekea ili ninyi mtukuzwe, kwa sababu naliwahubiri Injili ya Mungu bila ujira? 8 Naliwanyang'anya makanisa mengine mali yao, nikitwaa posho langu ili niwahudumie ninyi. 9 Nami nilipokuwa pamoja nanyi na kuhitaji sikumlemea mtu. Maana hao ndugu waliokuja kutoka Makedonia walinipa kadiri ya mahitaji yangu; nami katika mambo yote najilinda nafsi yangu nisiwalemee hata kidogo; tena najilinda. 10 Kama vile ile kweli ya Kristo ilivyo ndani yangu, hakuna mtu atakayenifumba kinywa katika kujisifu huku, katika mipaka ya Akaya. 11 Kwa nini? Je! Ni kwa sababu siwapendi ninyi? Mungu anajua. 12 Lakini nifanyalo nitalifanya, ili niwapinge hao watafutao nafasi wasipate nafasi; ili kwamba katika neno hilo wajisifialo waonekane kuwa kama sisi. 13 Maana watu kama hao ni mitume wa uongo, watendao kazi kwa hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo. 14 Wala si ajabu. Maana Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru. 15 Basi si neno kubwa watumishi wake nao wakijigeuza wawe mfano wa watumishi wa haki, ambao mwisho wao utakuwa sawasawa na kazi zao. 16 Nasema tena, mtu asidhani ya kuwa mimi ni mpumbavu; lakini mjaponidhania hivi, mnikubali kama mpumbavu; ili mimi nami nipate kujisifu ngaa kidogo. 17 Ninenalo silineni agizo la Bwana, bali kama kwa upumbavu, katika ujasiri huu wa kujisifu. 18 Kwa sababu wengi wanajisifu kwa jinsi ya mwili, mimi nami nitajisifu. 19 Ninyi, kwa kuwa mna akili, mnachukuliana na wajinga kwa furaha. 20 Maana mwachukuliana na mtu akiwatia utumwani, akiwameza, akiwateka nyara, akijikuza, akiwapiga usoni. 21 Nanena kwa jinsi ya kujidhili kana kwamba sisi tulikuwa dhaifu. Walakini, akiwa mtu anao ujasiri kwa lo lote, (nanena kipuuzi), mimi nami ninao ujasiri. 22 Wao ni Waebrania? Na mimi pia. Wao ni Waisraeli? Na mimi pia. Wao ni uzao wa Ibrahimu? Na mimi pia. 23 Wao ni wahudumu wa Kristo? (Nanena kiwazimu), mimi ni zaidi; katika taabu kuzidi sana; katika vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi. 24 Kwa Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. 25 Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi; kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; 26 katika kusafiri mara nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang'anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; 27 katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi. 28 Baghairi ya mambo ya nje, yako yanijiayo kila siku, ndiyo maangalizi ya makanisa yote. 29 Ni nani aliye dhaifu, nisiwe dhaifu nami? Ni nani aliyekwazwa nami nisichukiwe? 30 Ikinibidi kujisifu, nitajisifia mambo ya udhaifu wangu. 31 Mungu, Baba wa Bwana Yesu, aliye mtukufu hata milele, anajua ya kuwa sisemi uongo. 32 Huko Dameski liwali wa mfalme Areta alikuwa akiulinda mji wa Wadameski, ili kunikamata; 33 nami nikatelemshwa ndani ya kapu, katika dirisha la ukutani, nikaokoka katika mikono yake.

2 Wakorintho 12

1 Sina budi kujisifu, ijapokuwa haipendezi; lakini nitafikilia maono na mafunuo ya Bwana. 2 Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu. 3 Nami namjua mtu huyo, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua); 4 ya kuwa alinyakuliwa mpaka Peponi, akasikia maneno yasiyotamkika, ambayo haijuzu mwanadamu ayanene. 5 Kwa habari za mtu kama huyo nitajisifu; lakini kwa ajili ya nafsi yangu sitajisifu, isipokuwa katika habari ya udhaifu wangu. 6 Maana kama ningetaka kujisifu singekuwa mpumbavu, kwa sababu nitasema kweli. Lakini najizuia, ili mtu asinihesabie zaidi ya hayo ayaonayo kwangu au kuyasikia kwangu. 7 Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi. 8 Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke. 9 Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu. 10 Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu. 11 Nimekuwa mpumbavu, ninyi mmenilazimisha. Maana ilinipasa nisifiwe na ninyi; kwa sababu sikuwa duni ya mitume walio wakuu kwa lo lote, nijapokuwa si kitu. 12 Kweli ishara za mtume zilitendwa katikati yenu katika saburi yote, kwa ishara na maajabu na miujiza. 13 Maana ni kitu gani mlichopungukiwa kuliko makanisa mengine, ila kwa kuwa mimi sikuwalemea? Mnisamehe udhalimu huu. 14 Tazama, hii ni mara ya tatu ya mimi kuwa tayari kuja kwenu, wala sitawalemea. Maana sivitafuti vitu vyenu, bali nawatafuta ninyi; maana haiwapasi watoto kuweka akiba kwa wazazi, bali wazazi kwa watoto. 15 Nami kwa furaha nyingi nitatapanya, tena nitatapanywa kwa ajili ya roho zenu. Je! Kadiri nizidivyo kuwapenda sana, ninapungukiwa kupendwa? 16 Lakini na iwe hivyo, mimi sikuwalemea; bali kwa kuwa mwerevu naliwapata kwa hila. 17 Je! Mtu ye yote niliyemtuma kwenu, kwa mtu huyo naliwatoza kitu? 18 Nalimwonya Tito, nikamtuma ndugu yule pamoja naye. Je! Tito aliwatoza kitu? Je! Hatukuenenda kwa Roho yeye yule na katika nyayo zile zile? 19 Mwadhani hata sasa ya kuwa najidhuru kwenu! Mbele za Mungu twanena katika Kristo. Na hayo yote, wapenzi, ni kwa ajili ya kuwajenga ninyi. 20 Maana nachelea, nisije nikawakuta si kama vile nitakavyo kuwakuta, nikaonekana kwenu si kama vile mtakavyo; nisije nikakuta labda fitina na wivu, na ghadhabu, na ugomvi, na masingizio, na manong'onezo, na majivuno, na ghasia; 21 nami nitakapokuja tena, Mungu wangu asije akanidhili kwenu, nami nikawasikitikia wengi waliokosa tangu hapo, wasiutubie uchafu, na uasherati, na ufisadi walioufanya.

2 Wakorintho 13

1 Hii ndiyo mara ya tatu ya mimi kuja kwenu. Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno litathibitishwa. 2 Nimetangulia kuwaambia; na, kama vile nilipokuwapo mara ya pili, vivyo hivyo sasa nisipokuwapo, nawaambia wazi wao waliotenda dhambi tangu hapo, na wengine wote, ya kwamba, nikija, sitahurumia; 3 kwa kuwa mnatafuta dalili ya Kristo, asemaye ndani yangu, ambaye si dhaifu kwenu, bali ana uweza ndani yenu. 4 Maana, alisulibiwa katika udhaifu, lakini anaishi kwa nguvu za Mungu. Maana sisi nasi tu dhaifu katika yeye; lakini tutaishi pamoja naye kwa uweza wa Mungu ulio kwenu. 5 Jijaribuni wenyewe kwamba mmekuwa katika imani; jithibitisheni wenyewe. Au hamjijui wenyewe, kwamba Yesu Kristo yu ndani yenu? Isipokuwa mmekataliwa. 6 Lakini natumaini kama mtajua ya kuwa sisi hatukukataliwa. 7 Nasi twamwomba Mungu, msifanye lo lote lililo baya; si kwamba sisi tuonekane tumekubaliwa, lakini ninyi mfanye lile lililo jema, tujapokuwa sisi tu kama waliokataliwa. 8 Maana hatuwezi kutenda neno lo lote kinyume cha kweli, bali kwa ajili ya kweli. 9 Maana twafurahi, iwapo sisi tu dhaifu, nanyi mmekuwa hodari. Tena twaomba hili nalo, kutimilika kwenu. 10 Kwa sababu hiyo, naandika haya nisipokuwapo, ili, nikiwapo, nisiutumie ukali kwa kadiri ya uwezo ule niliopewa na Bwana, kwa kujenga wala si kwa kubomoa. 11 Hatimaye, ndugu, kwaherini; mtimilike, mfarijike, nieni mamoja, mkae katika amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi. 12 Salimianeni kwa busu takatifu. 13 Watakatifu wote wawasalimu. 14 Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu, na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote.

Wagalatia 1

1 Paulo, mtume, (si mtume wa wanadamu, wala kutumwa na mwanadamu, bali na Yesu Kristo, na Mungu Baba aliyemfufua kutoka kwa wafu), 2 na ndugu wote walio pamoja nami, kwa makanisa ya Galatia; 3 Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba, na kwa Bwana wetu Yesu Kristo; 4 ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili ya dhambi zetu, ili atuokoe na dunia hii mbovu iliyopo sasa, kama alivyopenda Mungu, Baba yetu. 5 Utukufu una yeye milele na milele, Amina. 6 Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia injili ya namna nyingine. 7 Wala si nyingine; lakini wapo watu wawataabishao na kutaka kuigeuza injili ya Kristo. 8 Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe. 9 Kama tulivyotangulia kusema, na sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo mliyoipokea, na alaaniwe. 10 Maana, sasa je! Ni wanadamu ninaowashawishi, au Mungu? Au nataka kuwapendeza wanadamu? Kama ningekuwa hata sasa nawapendeza wanadamu, singekuwa mtumwa wa Kristo. 11 Kwa maana, ndugu zangu, injili hiyo niliyowahubiri, nawajulisha ya kuwa siyo ya namna ya kibinadamu. 12 Kwa kuwa sikuipokea kwa mwanadamu wala sikufundishwa na mwanadamu, bali kwa ufunuo wa Yesu Kristo. 13 Maana mmesikia habari za mwenendo wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. 14 Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. 15 Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake, 16 alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu wenye mwili na damu; 17 wala sikupanda kwenda Yerusalemu kwa hao waliokuwa mitume kabla yangu; bali nalikwenda zangu Arabuni, kisha nikarudi tena Dameski. 18 Kisha, baada ya miaka mitatu, nalipanda kwenda Yerusalemu ili nionane na Kefa, nikakaa kwake siku kumi na tano. 19 Lakini sikumwona mtume mwingine, ila Yakobo, ndugu yake Bwana. 20 Na hayo ninayowaandikia, angalieni, mbele za Mungu, sisemi uongo. 21 Baadaye nalikwenda pande za Shamu na Kilikia. 22 Lakini sikujulikana uso wangu na makanisa ya Uyahudi yaliyokuwa katika Kristo; 23 ila wamesikia tu ya kwamba huyo aliyetuudhi hapo kwanza, sasa anaihubiri imani ile aliyoiharibu zamani. 24 Wakamtukuza Mungu kwa ajili yangu.

Wagalatia 2

1 Kisha, baada ya miaka kumi na minne, nalipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikamchukua na Tito pamoja nami. 2 Nami nalikwenda kwa kuwa nalifunuliwa, nikawaeleza injili ile niihubiriyo katika Mataifa, lakini kwa faragha kwa hao walio wenye sifa, isiwe labda napiga mbio bure, au nalipiga mbio bure. 3 Lakini Tito aliyekuwa pamoja nami, naye ni Myunani, hakulazimishwa kutahiriwa. 4 Bali kwa ajili ya ndugu za uongo walioingizwa kwa siri; ambao waliingia kwa siri ili kuupeleleza uhuru wetu tulio nao katika Kristo Yesu, ili watutie utumwani; 5 ambao hata saa moja hatukujitia chini yao, ili kwamba kweli ya Injili ikae pamoja nanyi. 6 Lakini wale wenye sifa ya kuwa wana cheo; (walivyokuwa vyo vyote ni mamoja kwangu; Mungu hapokei uso wa mwanadamu); nasema, hao wenye sifa hawakuniongezea kitu; 7 bali, kinyume cha hayo, walipoona ya kuwa nimekabidhiwa injili ya wasiotahiriwa, kama vile Petro ya waliotahiriwa; 8 (maana yeye aliyemwezesha Petro kuwa mtume wa waliotahiriwa ndiye aliyeniwezesha mimi kwenda kwa Mataifa); 9 tena walipokwisha kuijua ile neema niliyopewa; Yakobo, na Kefa, na Yohana, wenye sifa kuwa ni nguzo, walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika; ili sisi tuende kwa Mataifa, na wao waende kwa watu wa tohara; 10 ila neno moja tu walitutakia, tuwakumbuke maskini; nami neno lilo hilo nalikuwa na bidii kulifanya. 11 Lakini Kefa alipokuja Antiokia, nalishindana naye uso kwa uso, kwa sababu alistahili hukumu. 12 Kwa maana kabla hawajaja watu kadha wa kadha waliotoka kwa Yakobo, alikuwa akila pamoja na watu wa Mataifa; lakini walipokuja wao, akarudi nyuma akajitenga, huku akiwaogopa waliotahiriwa. 13 Na hao Wayahudi wengine wakajigeuza pamoja naye, hata na Barnaba pia akachukuliwa na unafiki wao. 14 Walakini, nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa mbele ya wote, Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa kufuata desturi za Wayahudi? 15 Sisi tulio Wayahudi kwa asili, wala si wakosaji wa Mataifa, 16 hali tukijua ya kuwa mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu; sisi tulimwamini Kristo Yesu ili tuhesabiwe haki kwa imani ya Kristo, wala si kwa matendo ya sheria; maana kwa matendo ya sheria hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki. 17 Lakini ikiwa sisi wenyewe, kwa kutafuta kuhesabiwa haki katika Kristo, tulionekana kuwa wenye dhambi, je! Kristo amekuwa mtumishi wa dhambi? Hasha! 18 Maana nikiyajenga tena yale niliyoyabomoa, naonyesha ya kuwa mimi mwenyewe ni mkosaji. 19 Maana mimi kwa njia ya sheria naliifia sheria ili nimwishie Mungu. 20 Nimesulibiwa pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu, ambaye alinipenda, akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu. 21 Siibatili neema ya Mungu; maana, ikiwa haki hupatikana kwa njia ya sheria, basi Kristo alikufa bure.

Wagalatia 3

1 Enyi Wagalatia msio na akili, ni nani aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo aliwekwa wazi mbele ya macho yenu ya kuwa amesulibiwa? 2 Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani? 3 Je! Mmekuwa wajinga namna hii? Baada ya kuanza katika Roho, mnataka kukamilishwa sasa katika mwili? 4 Mmepatikana na mateso makubwa namna hii bure? Ikiwa ni bure kweli. 5 Basi, yeye awapaye Roho na kufanya miujiza kati yenu, je! Afanya hayo kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani? 6 Kama vile Ibrahimu alivyomwamini Mungu akahesabiwa haki. 7 Fahamuni basi, ya kuwa wale walio wa imani, hao ndio wana wa Ibrahimu. 8 Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa. 9 Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani. 10 Kwa maana wale wote walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati, ayafanye. 11 Ni dhahiri ya kwamba hakuna mtu ahesabiwaye haki mbele za Mungu katika sheria; kwa sababu Mwenye haki ataishi kwa imani. 12 Na torati haikuja kwa imani, bali, Ayatendaye hayo ataishi katika hayo. 13 Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; 14 ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani. 15 Ndugu zangu, nanena kwa jinsi ya kibinadamu. Lijapokuwa ni agano la mwanadamu, hata hivyo likiisha kuthibitika, hakuna mtu alibatilishaye, wala kuliongeza neno. 16 Basi ahadi zilinenwa kwa Ibrahimu na kwa mzao wake. Hasemi, Kwa wazao, kana kwamba ni wengi, bali kana kwamba ni mmoja, Kwa mzao wako, yaani, Kristo. 17 Nisemalo ni hili; agano lililothibitishwa kwanza na Mungu, torati iliyotokea miaka mia nne na thelathini baadaye hailitangui, hata kuibatilisha ile ahadi. 18 Kwa maana urithi ukiwa kwa sheria, hauwi tena kwa ahadi; lakini Mungu alimkirimia Ibrahimu kwa njia ya ahadi. 19 Torati ni nini basi? Iliingizwa kwa sababu ya makosa, hata aje huyo mzao aliyepewa ile ahadi; iliamriwa kwa utumishi wa malaika kwa mkono wa mjumbe. 20 Basi aliye mjumbe si mjumbe wa mmoja; bali Mungu ni mmoja. 21 Basi je! Torati haipatani na ahadi za Mungu? Hasha! Kwa kuwa, kama ingalitolewa sheria iwezayo kuhuisha, yakini haki ingalipatikana kwa sheria. 22 Lakini andiko limeyafunga yote chini ya nguvu ya dhambi, makusudi hao waaminio wapewe ile ahadi kwa imani ya Yesu Kristo. 23 Lakini kabla ya kuja ile imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa. 24 Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. 25 Lakini, iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi. 26 Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu. 27 Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. 28 Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. 29 Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.

Wagalatia 4

1 Lakini nasema ya kuwa mrithi, wakati wote awapo mtoto, hana tofauti na mtumwa, angawa ni bwana wa yote; 2 bali yu chini ya mawakili na watunzaji, hata wakati uliokwisha kuamriwa na baba. 3 Kadhalika na sisi, tulipokuwa watoto, tulikuwa tukitumikishwa na kawaida za kwanza za dunia. 4 Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, 5 kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana. 6 Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba. 7 Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana; na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu. 8 Lakini wakati ule, kwa kuwa hamkumjua Mungu, mliwatumikia wao ambao kwa asili si miungu. 9 Bali sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini kuyarejea tena mafundisho ya kwanza yaliyo manyonge, yenye upungufu, ambayo mnataka kuyatumikia tena? 10 Mnashika siku, na miezi, na nyakati, na miaka. 11 Nawachelea, isiwe labda nimejitaabisha bure kwa ajili yenu. 12 Ndugu zangu, nawasihi, iweni kama mimi, maana mimi ni kama ninyi. Hamkunidhulumu kwa lo lote. 13 Lakini mwajua ya kuwa naliwahubiri Injili mara ya kwanza kwa sababu ya udhaifu wa mwili; 14 na jaribu lililowapata katika mwili wangu hamkulidharau wala kulikataa, bali mlinipokea kama malaika wa Mungu, kama Kristo Yesu. 15 Ku wapi, basi, kule kujiita heri? Maana nawashuhudu kwamba, kama ingaliwezekana, mngaling'oa macho yenu, mkanipa mimi. 16 Je! Nimekuwa adui wenu kwa sababu nawaambia yaliyo kweli? 17 Hao wana shauku nanyi, lakini si kwa njia nzuri, bali wanataka kuwafungia nje, ili kwamba ninyi mwaonee wao shauku. 18 Navyo ni vizuri kuonewa shauku katika neno jema sikuzote, wala si wakati nikiwapo mimi pamoja nanyi tu. 19 Vitoto vyangu, ambao kwamba nawaonea utungu tena mpaka Kristo aumbike ndani yenu; 20 laiti ningekuwapo pamoja nanyi sasa, na kuigeuza sauti yangu! Maana naona shaka kwa ajili yenu. 21 Niambieni, ninyi mnaotaka kuwa chini ya sheria, je! Hamwisikii sheria? 22 Kwa maana imeandikwa ya kuwa, Ibrahimu alikuwa na wana wawili mmoja kwa mjakazi, na mmoja kwa mwungwana. 23 Lakini yule wa mjakazi alizaliwa kwa mwili, yule wa mwungwana kwa ahadi. 24 Mambo haya husemwa kwa mfano; kwa maana hawa ndio kama maagano mawili, moja kutoka mlima Sinai, lizaalo kwa utumwa, ambalo ni Hajiri. 25 Maana Hajiri ni kama mlima Sinai ulioko Arabuni, umelingana na Yerusalemu wa sasa; kwa kuwa anatumika pamoja na watoto. 26 Bali Yerusalemu wa juu ni mwungwana, naye ndiye mama yetu sisi. 27 Kwa maana imeandikwa, Furahi, wewe uliye tasa, usiyezaa; Paza sauti, ulie, wewe usiye na utungu; Maana watoto wake aliyeachwa pekee ni wengi Kuliko wa huyo aliye na mume. 28 Basi, ndugu zangu, kama Isaka sisi tu watoto wa ahadi. 29 Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa. 30 Lakini lasemaje andiko? Mfukuze mjakazi na mwanawe, kwa maana mwana wa mjakazi hatarithi kabisa pamoja na mwana wa mwungwana. 31 Ndiposa, ndugu zangu, sisi si watoto wa mjakazi, bali tu watoto wa huyo aliye mwungwana.

Wagalatia 5

1 Katika ungwana huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa. 2 Tazama, mimi Paulo nawaambia ninyi ya kwamba, mkitahiriwa, Kristo hatawafaidia neno. 3 Tena namshuhudia kila mtu atahiriwaye, kwamba ni wajibu wake kuitimiza torati yote. 4 Mmetengwa na Kristo, ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema. 5 Maana sisi kwa Roho tunalitazamia tumaini la haki kwa njia ya imani. 6 Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa upendo. 7 Mlikuwa mkipiga mbio vizuri; ni nani aliyewazuia msiitii kweli? 8 Kushawishi huku hakukutoka kwake yeye anayewaita ninyi. 9 Chachu kidogo huchachua donge zima. 10 Nina matumaini kwenu katika Bwana, ya kwamba hamtakuwa na nia ya namna nyingine. Lakini yeye anayewafadhaisha atachukua hukumu yake, awaye yote. 11 Nami, ndugu zangu ikiwa ninahubiri habari ya kutahiriwa, kwa nini ningali ninaudhiwa? Hapo kwazo la msalaba limebatilika! 12 Laiti hao wanaowatia mashaka wangejikata nafsi zao! 13 Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo. 14 Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako. 15 Lakini mkiumana na kulana, angalieni msije mkaangamizana. 16 Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. 17 Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. 18 Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. 19 Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, 20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, 21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. 22 Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, 23 upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. 24 Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. 25 Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho. 26 Tusijisifu bure, tukichokozana na kuhusudiana.

Wagalatia 6

1 Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe. 2 Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo. 3 Maana mtu akijiona kuwa ni kitu, naye si kitu, ajidanganya nafsi yake. 4 Lakini kila mtu na aipime kazi yake mwenyewe, ndipo atakapokuwa na sababu ya kujisifu ndani ya nafsi yake tu, wala si kwa mwenzake. 5 Maana kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe. 6 Mwanafunzi na amshirikishe mkufunzi wake katika mema yote. 7 Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. 8 Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna uzima wa milele. 9 Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho. 10 Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio. 11 Tazameni ni kwa herufi gani kubwa nimewaandikia kwa mkono wangu mimi mwenyewe! 12 Wote watakao kuonekana ni wazuri kwa mambo ya mwili, ndio wanaowashurutisha kutahiriwa; makusudi wasiudhiwe kwa ajili ya msalaba wa Kristo, hilo tu. 13 Kwa maana hata wao wenyewe waliotahiriwa hawaishiki sheria; bali wanataka ninyi mtahiriwe, wapate kuona fahari katika miili yenu. 14 Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu. 15 Kwa sababu kutahiriwa si kitu, wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya. 16 Na wote watakaoenenda kwa kanuni hiyo, amani na iwe kwao na rehema, naam, kwa Israeli wa Mungu. 17 Tangu sasa mtu asinitaabishe; kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu. 18 Ndugu zangu, neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu. Amina.

Waefeso 1

1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu, kwa mapenzi ya Mungu; kwa watakatifu walioko Efeso wanaomwamini Kristo Yesu. 2 Neema na iwe kwenu na amani zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. 3 Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo; 4 kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo. 5 Kwa kuwa alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake. 6 Na usifiwe utukufu wa neema yake, ambayo ametuneemesha katika huyo Mpendwa. 7 Katika yeye huyo, kwa damu yake, tunao ukombozi wetu, masamaha ya dhambi, sawasawa na wingi wa neema yake. 8 Naye alituzidishia hiyo katika hekima yote na ujuzi; 9 akiisha kutujulisha siri ya mapenzi yake, sawasawa na uradhi wake, alioukusudia katika yeye huyo. 10 Yaani, kuleta madaraka ya wakati mkamilifu atavijumlisha vitu vyote katika Kristo, vitu vya mbinguni na vitu vya duniani pia. Naam, katika yeye huyo; 11 na ndani yake sisi nasi tulifanywa urithi, huku tukichaguliwa tangu awali sawasawa na kusudi lake yeye, ambaye hufanya mambo yote kwa shauri la mapenzi yake. 12 Nasi katika huyo tupate kuwa sifa ya utukufu wake, sisi tuliotangulia kumwekea Kristo tumaini letu. 13 Nanyi pia katika huyo mmekwisha kulisikia neno la kweli, habari njema za wokovu wenu; tena mmekwisha kumwamini yeye, na kutiwa muhuri na Roho yule wa ahadi aliye Mtakatifu. 14 Ndiye aliye arabuni ya urithi wetu, ili kuleta ukombozi wa milki yake, kuwa sifa ya utukufu wake. 15 Kwa sababu hiyo mimi nami, tangu nilipopata habari za imani yenu katika Bwana Yesu, na pendo lenu kwa watakatifu wote, 16 siachi kutoa shukrani kwa ajili yenu; nikiwakumbuka katika sala zangu, 17 Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; 18 macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo; 19 na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; 20 aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; 21 juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; 22 akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo 23 ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.

Waefeso 2

1 Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; 2 ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; 3 ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine. 4 Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda; 5 hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema. 6 Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu; 7 ili katika zamani zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi katika Kristo Yesu. 8 Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; 9 wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu. 10 Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo. 11 Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono; 12 kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani. 13 Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo. 14 Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga. 15 Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani. 16 Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuufisha ule uadui kwa huo msalaba. 17 Akaja akahubiri amani kwenu ninyi mliokuwa mbali, na amani kwao wale waliokuwa karibu. 18 Kwa maana kwa yeye sisi sote tumepata njia ya kumkaribia Baba katika Roho mmoja. 19 Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu. 20 Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. 21 Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana. 22 Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho.

Waefeso 3

1 Kwa sababu hiyo mimi Paulo ni mfungwa wake Kristo Yesu kwa ajili yenu ninyi Mataifa; 2 ikiwa mmesikia habari ya uwakili wa neema ya Mungu niliyopewa kwa ajili yenu; 3 ya kwamba kwa kufunuliwa nalijulishwa siri hiyo, kama nilivyotangulia kuandika kwa maneno machache. 4 Kwa hayo, myasomapo, mtaweza kuutambua ufahamu wangu katika siri yake Kristo. 5 Siri hiyo hawakujulishwa wanadamu katika vizazi vingine; kama walivyofunuliwa mitume wake watakatifu na manabii zamani hizi katika Roho; 6 ya kwamba Mataifa ni warithi pamoja nasi wa urithi mmoja, na wa mwili mmoja, na washiriki pamoja nasi wa ahadi yake iliyo katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili; 7 Injili hiyo ambayo nalifanywa mhudumu wake, kwa kadiri ya kipawa cha neema ya Mungu niliyopewa kwa kadiri ya utendaji wa uweza wake. 8 Mimi, niliye mdogo kuliko yeye aliye mdogo wa watakatifu wote, nalipewa neema hii ya kuwahubiri Mataifa utajiri wake Kristo usiopimika; 9 na kuwaangaza watu wote wajue habari za madaraka ya siri hiyo, ambayo tangu zamani zote ilisitirika katika Mungu aliyeviumba vitu vyote; 10 ili sasa, kwa njia ya kanisa, hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi ijulikane na falme na mamlaka katika ulimwengu wa roho; 11 kwa kadiri ya kusudi la milele alilolikusudia katika Kristo Yesu Bwana wetu. 12 Katika yeye tunao ujasiri na uwezo wa kukaribia katika tumaini kwa njia ya kumwamini. 13 Basi naomba msikate tamaa kwa sababu ya dhiki zangu kwa ajili yenu, zilizo utukufu kwenu. 14 Kwa hiyo nampigia Baba magoti, 15 ambaye kwa jina lake ubaba wote wa mbinguni na wa duniani unaitwa, 16 awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake katika utu wa ndani. 17 Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; 18 ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo, na kina; 19 na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu. 20 Basi atukuzwe yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo, kwa kadiri ya nguvu itendayo kazi ndani yetu; 21 naam, atukuzwe katika Kanisa na katika Kristo Yesu hata vizazi vyote vya milele na milele. Amina.

Waefeso 4

1 Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, mwenende kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; 2 kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; 3 na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani. 4 Mwili mmoja, na Roho mmoja, kama na mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu. 5 Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. 6 Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote. 7 Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. 8 Hivyo husema, Alipopaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa. 9 Basi neno hilo, Alipaa, maana yake nini kama siyo kusema kwamba yeye naye alishuka mpaka pande zilizo chini za nchi? 10 Naye aliyeshuka ndiye yeye aliyepaa juu sana kupita mbingu zote, ili avijaze vitu vyote. 11 Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; 12 kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; 13 hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; 14 ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu. 15 Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. 16 Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu moja moja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo. 17 Basi nasema neno hili, tena nashuhudia katika Bwana, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; 18 ambao; akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao; 19 ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani. 20 Bali ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; 21 ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo katika Yesu, 22 mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; 23 na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; 24 mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli. 25 Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake; kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake. 26 Mwe na hasira, ila msitende dhambi; jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka; 27 wala msimpe Ibilisi nafasi. 28 Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji. 29 Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia. 30 Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi. 31 Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; 32 tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.

Waefeso 5

1 Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; 2 mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato. 3 Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wa kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; 4 wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru. 5 Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu. 6 Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa kwa sababu ya hayo hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi. 7 Basi msishirikiane nao. 8 Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru, 9 kwa kuwa tunda la nuru ni katika wema wote na haki na kweli; 10 mkihakiki ni nini impendezayo Bwana. 11 Wala msishirikiane na matendo yasiyozaa ya giza, bali myakemee; 12 kwa kuwa yanayotendeka kwao kwa siri, ni aibu hata kuyanena. 13 Lakini yote yaliyokemewa hudhihirishwa na nuru maana kila kilichodhihirika ni nuru. 14 Hivyo husema, Amka, wewe usinziaye, Ufufuke katika wafu, Na Kristo atakuangaza. 15 Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; 16 mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. 17 Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana. 18 Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; bali mjazwe Roho; 19 mkisemezana kwa zaburi na tenzi na nyimbo za rohoni, huku mkiimba na kumshangilia Bwana mioyoni mwenu; 20 na kumshukuru Mungu Baba sikuzote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo; 21 hali mnanyenyekeana katika kicho cha Kristo. 22 Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. 23 Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. 24 Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo. 25 Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; 26 ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; 27 apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa. 28 Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. 29 Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa. 30 Kwa kuwa tu viungo vya mwili wake. 31 Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja. 32 Siri hiyo ni kubwa; ila mimi nanena habari ya Kristo na Kanisa. 33 Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe.

Waefeso 6

1 Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki. 2 Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, 3 Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia. 4 Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana. 5 Enyi watumwa, watiini wao walio bwana zenu kwa jinsi ya mwili, kwa hofu na kutetemeka, kwa unyofu wa moyo, kana kwamba ni kumtii Kristo; 6 wala si kwa utumwa wa macho tu kama wajipendekazao kwa wanadamu bali kama watumwa wa Kristo, mkitenda yampendezayo Mungu kwa moyo; 7 kwa nia njema kama kumtumikia Bwana wala si mwanadamu; 8 mkijua ya kuwa kila neno jema alitendalo mtu atapewa lilo hilo na Bwana kwamba ni mtumwa au kwamba ni huru. 9 Nanyi, akina bwana, watendeeni wao yayo hayo, mkiacha kuwaogofya, huku mkijua ya kuwa yeye aliye Bwana wao na wenu yuko mbinguni, wala kwake hakuna upendeleo. 10 Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. 11 Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. 12 Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. 13 Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. 14 Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, 15 na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; 16 zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. 17 Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; 18 kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; 19 pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili; 20 ambayo kwa ajili yake mimi ni mjumbe katika minyororo; hata nipate ujasiri katika huyo kunena jinsi inipasavyo kunena. 21 Basi ninyi nanyi mpate kuzijua habari zangu, ni hali gani, Tikiko, ndugu mpendwa, mhudumu mwaminifu katika Bwana, atawajulisheni mambo yote; 22 ambaye nampeleka kwenu kwa kusudi lilo hilo mpate kuzijua habari zetu, naye awafariji mioyo yenu. 23 Amani na iwe kwa ndugu, na pendo, pamoja na imani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Bwana Yesu Kristo. 24 Neema na iwe pamoja na wote wampendao Bwana wetu Yesu Kristo katika hali ya kutokuharibika.

Wafilipi 1

1 Paulo na Timotheo, watumwa wa Kristo Yesu, kwa watakatifu wote katika Kristo Yesu, walioko Filipi, pamoja na maaskofu na mashemasi. 2 Neema na iwe kwenu na amani zitokazo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. 3 Namshukuru Mungu wangu kila niwakumbukapo, 4 sikuzote kila niwaombeapo ninyi nyote nikisema sala zangu kwa furaha, 5 kwa sababu ya ushirika wenu katika kuieneza Injili, tangu siku ile ya kwanza hata leo hivi. 6 Nami niliaminilo ndilo hili, ya kwamba yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza hata siku ya Kristo Yesu; 7 vile vile kama ilivyo wajibu wangu kufikiri haya juu yenu nyote; kwa sababu ninyi mmo moyoni mwangu; kwa kuwa katika kufungwa kwangu na katika kazi ya kutetea Injili na kuithibitisha, ninyi nyote mmeshirikiana nami neema hii. 8 Maana Mungu ni shahidi wangu, jinsi ninavyowaonea shauku ninyi nyote katika moyo wake Kristo Yesu. 9 Na hii ndiyo dua yangu, kwamba pendo lenu lizidi kuwa jingi sana, katika hekima na ufahamu wote; 10 mpate kuyakubali yaliyo mema; ili mpate kuwa na mioyo safi, bila kosa, mpaka siku ya Kristo; 11 hali mmejazwa matunda ya haki, kwa njia ya Yesu Kristo, kwa utukufu na sifa ya Mungu. 12 Lakini, ndugu zangu, nataka mjue ya kuwa mambo yote yaliyonipata yametokea zaidi kwa kuieneza Injili; 13 hata vifungo vyangu vimekuwa dhahiri katika Kristo, miongoni mwa askari, na kwa wengine wote pia. 14 Na wengi wa hao ndugu walio katika Bwana, hali wakapata kuthibitika kwa ajili ya kufungwa kwangu, wamezidi sana kuthubutu kunena neno la Mungu pasipo hofu. 15 Wengine wanahubiri habari za Kristo kwa sababu ya husuda na fitina; na wengine kwa nia njema. 16 Hawa wanamhubiri kwa pendo, wakijua ya kuwa nimewekwa ili niitetee Injili; 17 bali wengine wanamhubiri Kristo kwa fitina, wala si kwa moyo mweupe, wakidhani kuongeza dhiki za kufungwa kwangu. 18 Yadhuru nini? Lakini kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi. 19 Maana najua ya kuwa haya yatanigeukia kuwa wokovu wangu, kwa sababu ya kuomba kwenu, na kuruzukiwa Roho wa Yesu Kristo; 20 kama vile nilivyotazamia sana, na kutumaini, kwamba sitaaibika kamwe, bali kwa uthabiti wote, kama sikuzote na sasa vivyo hivyo Kristo ataadhimishwa katika mwili wangu; ikiwa kwa maisha yangu, au ikiwa kwa mauti yangu. 21 Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida. 22 Ila ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui. 23 Ninasongwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo maana ni vizuri zaidi sana; 24 bali kudumu katika mwili kwahitajiwa zaidi kwa ajili yenu. 25 Nami nikitumaini hayo, najua ya kuwa nitakaa na kudumu pamoja nanyi, ili mpate kuendelea na kufurahi katika imani; 26 hata mzidi kuona fahari katika Kristo Yesu juu yangu kwa sababu ya kuwapo kwangu pamoja nanyi tena. 27 Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo, ili, nikija na kuwaona ninyi, au nisipokuwapo, niyasikie mambo yenu, kama mnasimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili; 28 wala hamwaogopi adui zenu, katika neno lo lote; kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ninyi ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa Mungu. 29 Maana mmepewa kwa ajili ya Kristo, si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake; 30 mkiwa na mashindano yale yale mliyoyaona kwangu, na kusikia kwamba ninayo hata sasa.

Wafilipi 2

1 Basi ikiwako faraja yo yote katika Kristo, yakiwako matulizo yo yote ya mapenzi, ukiwako ushirika wo wote wa Roho, ikiwako huruma yo yote na rehema, 2 ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja, wenye roho moja, mkinia mamoja. 3 Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. 4 Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine. 5 Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; 6 ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; 7 bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; 8 tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. 9 Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; 10 ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; 11 na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba. 12 Basi, wapendwa wangu, kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka. 13 Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema. 14 Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, 15 mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu, 16 mkishika neno la uzima; nipate sababu ya kuona fahari katika siku ya Kristo, ya kuwa sikupiga mbio bure wala sikujitaabisha bure. 17 Naam, hata nikimiminwa juu ya dhabihu na ibada ya imani yenu, nafurahi; tena nafurahi pamoja nanyi nyote. 18 Nanyi vivyo hivyo furahini, tena furahini pamoja nami. 19 Walakini natumaini katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo afike kwenu karibu, nifarijiwe na mimi, nikiijua hali yenu. 20 Maana sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. 21 Maana wote wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu. 22 Ila mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili, kama mwana na baba yake. 23 Basi, natumaini kumtuma huyo mara, hapo nitakapojua yatakayonipata. 24 Nami naamini katika Bwana ya kuwa nitakuja na mimi mwenyewe hivi karibu. 25 Lakini naliona imenilazimu kumtuma kwenu Epafrodito, ndugu yangu, mtenda kazi pamoja nami, askari pamoja nami; tena ni mtume wenu na mhudumu wa mahitaji yangu. 26 Kwa kuwa alikuwa na shauku kwenu ninyi nyote, akahuzunika sana, kwa sababu mlisikia ya kwamba alikuwa hawezi. 27 Kwa maana alikuwa hawezi kweli kweli, karibu na kufa; lakini Mungu alimhurumia; wala si yeye peke yake, ila na mimi pia; nisiwe na huzuni juu ya huzuni. 28 Kwa hiyo nimefanya bidii nyingi zaidi kumtuma, ili mtakapomwona tena mpate kufurahi, nami nipunguziwe huzuni yangu. 29 Mpokeeni, basi, katika Bwana, kwa furaha yote, mkawahesabu watu kama huyu kuwa watu wa kuheshimiwa. 30 Maana kwa ajili ya kazi ya Kristo alikaribia kufa akaponza roho yake; ili kusudi ayatimize yaliyopungua katika huduma yenu kwangu.

Wafilipi 3

1 Hatimaye, ndugu zangu, furahini katika Bwana. Kuwaandikieni mambo yale yale hakuniudhi mimi, bali kutawafaa ninyi. 2 Jihadharini na mbwa, jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao. 3 Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili. 4 Walakini mimi ningeweza kuutumainia mwili. Mtu ye yote akijiona kuwa anayo sababu ya kuutumainia mwili, mimi zaidi. 5 Nalitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila ya Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo, 6 kwa habari ya juhudi, mwenye kuliudhi Kanisa, kwa habari ya haki ipatikanayo kwa sheria sikuwa na hatia. 7 Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo. 8 Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo; 9 tena nionekane katika yeye, nisiwe na haki yangu mwenyewe ipatikanayo kwa sheria, bali ile ipatikanayo kwa imani iliyo katika Kristo, haki ile itokayo kwa Mungu, kwa imani; 10 ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake; 11 ili nipate kwa njia yo yote kuifikia kiyama ya wafu. 12 Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. 13 Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; 14 nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu. 15 Basi sisi tulio wakamilifu na tuwaze hayo; na hata mkiwaza mengine katika jambo lo lote, Mungu atawafunulia hilo nalo. 16 Lakini, hapo tulipofika na tuenende katika lilo hilo. 17 Ndugu zangu, mnifuate mimi, mkawatazame wao waendao kwa kuufuata mfano tuliowapa ninyi. 18 Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo; 19 mwisho wao ni uharibifu, mungu wao ni tumbo, utukufu wao u katika fedheha yao, waniao mambo ya duniani. 20 Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo; 21 atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake.

Wafilipi 4

1 Basi, ndugu zangu, wapendwa wangu, ninaowaonea shauku, furaha yangu, na taji yangu, hivyo simameni imara katika Bwana, wapenzi wangu. 2 Namsihi Euodia, namsihi na Sintike, wawe na nia moja katika Bwana. 3 Naam, nataka na wewe pia, mjoli wa kweli, uwasaidie wanawake hao; kwa maana waliishindania Injili pamoja nami, na Klementi naye, na wale wengine waliotenda kazi pamoja nami, ambao majina yao yamo katika kitabu cha uzima. 4 Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini. 5 Upole wenu na ujulikane na watu wote. Bwana yu karibu. 6 Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. 7 Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu. 8 Hatimaye, ndugu zangu, mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo. 9 Mambo mliyojifunza kwangu na kuyapokea, na kuyasikia na kuyaona kwangu, yatendeni hayo; na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi. 10 Nalifurahi sana katika Bwana, kwa kuwa sasa mwisho mmehuisha tena fikira zenu kwa ajili yangu, kama vile mlivyokuwa mkinifikiri hali yangu lakini hamkupata nafasi. 11 Si kwamba nasema haya kwa kuwa nina mahitaji; maana nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo. 12 Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. 13 Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu. 14 Lakini mlifanya vema, mliposhiriki nami katika dhiki yangu. 15 Nanyi pia, ninyi wenyewe mnajua, enyi Wafilipi, ya kuwa katika mwanzo wa Injili, nilipotoka Makedonia, hakuna kanisa lingine lililoshirikiana nami katika habari hii ya kutoa na kupokea, ila ninyi peke yenu. 16 Kwa kuwa hata huko Thesalonike mliniletea msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja. 17 Si kwamba nakitamani kile kipawa, bali nayatamani mazao yanayozidi kuwa mengi, katika hesabu yenu. 18 Lakini ninavyo vitu vyote na kuzidi, tena nimejaa tele; nimepokea kwa mkono wa Epafrodito vitu vile vilivyotoka kwenu, harufu ya manukato, sadaka yenye kibali, impendezayo Mungu. 19 Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu. 20 Sasa atukuzwe Mungu, Baba yetu, milele na milele. Amina. 21 Mnisalimie kila mtakatifu katika Kristo Yesu. Ndugu walio pamoja nami wawasalimu. 22 Watakatifu wote wawasalimu, hasa wao walio wa nyumbani mwa Kaisari. 23 Neema ya Bwana Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu.

Wakolosai 1

1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu, na Timotheo, ndugu yetu, 2 kwa ndugu watakatifu, waaminifu katika Kristo, walioko Kolosai. Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu. 3 Twamshukuru Mungu, Baba yake Bwana wetu Yesu Kristo, siku zote tukiwaombea; 4 tangu tuliposikia habari za imani yenu katika Kristo Yesu, na upendo mlio nao kwa watakatifu wote; 5kwa sababu ya tumaini mlilowekewa akiba mbinguni; ambalo habari zake mlizisikia zamani kwa neno la kweli ya Injili; 6 iliyofika kwenu, kama ilivyo katika ulimwengu wote, na kuzaa matunda na kukua, kama inavyokua kwenu pia, tangu siku mlipoisikia mkaifahamu sana neema ya Mungu katika kweli; 7 kama mlivyofundishwa na Epafra, mjoli wetu mpenzi, aliye mhudumu mwaminifu wa Kristo kwa ajili yenu; 8 naye alitueleza upendo wenu katika Roho. 9 Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; 10 mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; 11 mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; 12 mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru. 13 Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; 14 ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi; 15 naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. 16 Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake. 17 Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye. 18 Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa; naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote. 19 Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; 20 na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni. 21 Na ninyi, mliokuwa hapo kwanza mmefarikishwa, tena adui katika nia zenu, kwa matendo yenu mabaya, amewapatanisha sasa; 22 katika mwili wa nyama yake, kwa kufa kwake, ili awalete ninyi mbele zake, watakatifu, wasio na mawaa wala lawama; 23 mkidumu tu katika ile imani, hali mmewekwa juu ya msingi, mkawa imara; msipogeuzwa na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu; ambayo mimi Paulo nalikuwa mhudumu wake. 24 Sasa nayafurahia mateso niliyo nayo kwa ajili yenu; tena nayatimiliza katika mwili wangu yale yaliyopungua ya mateso ya Kristo, kwa ajili ya mwili wake, yaani, kanisa lake; 25 ambalo nimefanywa mhudumu wake, sawasawa na uwakili wa Mungu, niliopewa kwa faida yenu, nilitimize neno la Mungu; 26 siri ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake; 27 ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa siri hii katika Mataifa, nao ni Kristo ndani yenu, tumaini la utukufu 28 ambaye sisi tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo. 29 Nami najitaabisha kwa neno lilo hilo, nikijitahidi kwa kadiri ya kutenda kazi kwake atendaye kazi ndani yangu kwa nguvu.

Wakolosai 2

1 Maana nataka ninyi mjue jinsi ilivyo kuu juhudi yangu niliyo nayo kwa ajili yenu, na kwa ajili ya wale wa Laodikia, na wale wasioniona uso wangu katika mwili; 2 ili wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo, wakapate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani, Kristo; 3 ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika. 4 Nasema neno hili, mtu asije akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. 5 Maana nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo. 6 Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye; 7 wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani. 8 Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo. 9 Maana katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili. 10 Na ninyi mmetimilika katika yeye aliye kichwa cha enzi yote na mamlaka. 11 Katika yeye mmetahiriwa kwa tohara isiyofanyika kwa mikono, kwa kuuvua mwili wa nyama, kwa tohara ya Kristo. 12 Mkazikwa pamoja naye katika ubatizo; na katika huo mkafufuliwa pamoja naye, kwa kuziamini nguvu za Mungu aliyemfufua katika wafu. 13 Na ninyi mlipokuwa mmekufa kwa sababu ya makosa yenu na kutokutahiriwa kwa mwili wenu, aliwafanya hai pamoja naye, akiisha kutusamehe makosa yote; 14 akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; 15 akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo. 16 Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; 17 mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo. 18 Mtu asiwanyang'anye thawabu yenu, kwa kunyenyekea kwa mapenzi yake mwenyewe tu, na kuabudu malaika, akijitia katika maono yake na kujivuna bure, kwa akili zake za kimwili; 19 wala hakishiki Kichwa, ambacho kwa yeye mwili wote ukiruzukiwa na kuungamanishwa kwa viungo na mishipa, hukua kwa maongeo yatokayo kwa Mungu. 20 Basi ikiwa mlikufa pamoja na Kristo mkayaacha yale mafundisho ya awali ya ulimwengu, kwa nini kujitia chini ya amri, kama wenye kuishi duniani, 21 Msishike, msionje, msiguse; 22 (mambo hayo yote huharibika wakati wa kutumiwa); hali mkifuata maagizo na mafundisho ya wanadamu? 23 Mambo hayo yanaonekana kana kwamba yana hekima, katika namna ya ibada mliyojitungia wenyewe, na katika kunyenyekea, na katika kuutawala mwili kwa ukali; lakini hayafai kitu kwa kuzizuia tamaa za mwili.

Wakolosai 3

1 Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. 2 Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi. 3 Kwa maana mlikufa, na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. 4 Kristo atakapofunuliwa, aliye uhai wetu, ndipo na ninyi mtafunuliwa pamoja naye katika utukufu. 5 Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu; 6 kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu. 7 Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. 8 Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu. 9 Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; 10 mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba. 11 Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote. 12 Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, 13 mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. 14 Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu. 15 Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani. 16 Neno la Kristo na likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, mkifundishana na kuonyana kwa zaburi, na nyimbo, na tenzi za rohoni; huku mkimwimbia Mungu kwa neema mioyoni mwenu. 17 Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye. 18 Ninyi wake, watiini waume zenu, kama ipendezavyo katika Bwana. 19 Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao. 20 Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana. 21 Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa. 22 Ninyi watumwa, watiini hao ambao kwa mwili ni bwana zenu, katika mambo yote, si kwa utumwa wa macho, kama wajipendekezao kwa wanadamu, bali kwa unyofu wa moyo, mkimcha Bwana. 23 Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu, 24 mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi. Mnamtumikia Bwana Kristo. 25 Maana adhulumuye atapata mapato ya udhalimu wake, wala hakuna upendeleo.

Wakolosai 4

1 Ninyi akina bwana, wapeni watumwa wenu yaliyo haki na ya adili, mkijua ya kuwa ninyi nanyi mna Bwana mbinguni. 2 Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; 3 mkituombea na sisi pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa, 4 ili niidhihirishe, kama inipasavyo kunena. 5 Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati. 6 Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu. 7 Tikiko, ndugu mpendwa, mtumishi mwaminifu, mjoli wangu katika Bwana, atawaarifu mambo yangu yote; 8 ambaye nimemtuma kwenu kwa sababu iyo hiyo, ili mjue mambo yetu, naye akawafariji mioyo yenu; 9 pamoja na Onesimo, ndugu mwaminifu, mpendwa, aliye mtu wa kwenu. Hao watawaarifu mambo yote ya hapa petu. 10 Aristarko, aliyefungwa pamoja nami, awasalimu; na Marko, mjomba wake Barnaba, ambaye mmepokea maagizo kwa habari yake; akifika kwenu mkaribisheni. 11 Na Yesu aitwaye Yusto; hao ni watu wa tohara. Tena hao peke yao ni watendaji wa kazi pamoja nami kwa ajili ya ufalme wa Mungu; nao walikuwa faraja kwangu. 12 Epafra, aliye mtu wa kwenu, mtumwa wa Yesu Kristo, awasalimu, akifanya bidii siku zote kwa ajili yenu katika maombi yake, ili kwamba msimame wakamilifu na kuthibitika sana katika mapenzi yote ya Mungu. 13 Maana namshuhudia kwamba ana juhudi nyingi kwa ajili yenu, na kwa ajili ya hao walioko Laodikia, na kwa ajili ya hao walioko Hierapoli. 14 Luka, yule tabibu mpendwa, na Dema, wanawasalimu. 15 Wasalimuni ndugu walioko Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. 16 Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi. 17 Mwambieni Arkipo, Iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize. 18 Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.

1 Wathesalonike 1

1 Paulo, na Silwano, na Timotheo, kwa kanisa la Wathesalonike, lililo katika Mungu Baba, na katika Bwana Yesu Kristo. Neema na iwe kwenu na amani. 2 Twamshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu nyote, tukiwataja katika maombi yetu. 3 Wala hatuachi kuikumbuka kazi yenu ya imani, na taabu yenu ya upendo, na saburi yenu ya tumaini lililo katika Bwana wetu Yesu Kristo, mbele za Mungu Baba yetu. 4 Kwa maana, ndugu mnaopendwa na Mungu, twajua uteule wenu; 5 ya kwamba injili yetu haikuwafikia katika maneno tu, bali na katika nguvu, na katika Roho Mtakatifu, na uthibitifu mwingi; kama vile mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu. 6 Nanyi mkawa wafuasi wetu na wa Bwana, mkiisha kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na furaha ya Roho Mtakatifu. 7 Hata mkawa kielelezo kwa watu wote waaminio katika Makedonia, na katika Akaya. 8 Maana kutoka kwenu neno la Mungu limevuma, si katika Makedonia na Akaya tu, ila na kila mahali imani yenu mliyo nayo kwa Mungu imeenea; hata hatuna haja sisi kunena lo lote. 9 Kwa kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu aliye hai, wa kweli; 10 na kumngojea Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu, mwenye kutuokoa na ghadhabu itakayokuja.

1 Wathesalonike 2

1 Maana ninyi wenyewe, ndugu, mwakujua kuingia kwetu kwenu, ya kwamba hakukuwa bure; 2 lakini tukiisha kuteswa kwanza na kutendwa jeuri, kama mjuavyo, katika Filipi, twalithubutu katika Mungu kuinena Injili ya Mungu kwenu, kwa kuishindania sana. 3 Kwa maana maonyo yetu siyo ya ukosefu, wala ya uchafu, wala ya hila; 4 bali kama vile tulivyopata kibali kwa Mungu tuwekewe amana Injili, ndivyo tunenavyo; si kama wapendezao wanadamu, bali wampendezao Mungu anayetupima mioyo yetu. 5 Maana hatukuwa na maneno ya kujipendekeza wakati wo wote, kama mjuavyo, wala maneno ya juujuu ya kuficha choyo; Mungu ni shahidi. 6 Hatukutafuta utukufu kwa wanadamu, wala kwenu, wala kwa wengine tulipokuwa tukiweza kuwalemea kama mitume wa Kristo; 7 bali tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. 8 Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu. 9 Maana, ndugu, mnakumbuka taabu yetu na masumbufu yetu; kwa kuwa mchana na usiku tulifanya kazi tusije tukamlemea mtu wa kwenu awaye yote, tukawahubiri hivi Injili ya Mungu. 10 Ninyi ni mashahidi, na Mungu pia, jinsi tulivyokaa kwenu ninyi mnaoamini, kwa utakatifu, na kwa haki, bila kulaumiwa; 11 vile vile, kama mjuavyo, jinsi tulivyomwonya kila mmoja wenu kama baba awaonyavyo watoto wake mwenyewe, tukiwatia moyo na kushuhudia; 12 ili mwenende kama ilivyo wajibu wenu kwa Mungu, mwenye kuwaita ninyi ili mwingie katika ufalme wake na utukufu wake. 13 Kwa sababu hiyo sisi nasi twamshukuru Mungu bila kukoma, kwa kuwa, mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli; litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini. 14 Maana ninyi, ndugu, mlikuwa wafuasi wa makanisa ya Mungu yaliyo katika Uyahudi, katika Kristo Yesu; kwa kuwa mlipata mateso yale yale kwa watu wa taifa lenu wenyewe, waliyoyapata na hao kwa Wayahudi; 15 ambao walimwua Bwana Yesu, na hao manabii, na kutuudhi sisi; wala hawampendezi Mungu, wala hawapatani na watu wo wote; 16 huku wakituzuia tusiseme na Mataifa wapate kuokolewa; ili watimize dhambi zao siku zote. Lakini hasira imewafikia hata mwisho. 17 Lakini sisi, ndugu, tukiwa tumefarakana nanyi kwa kitambo, kwa uso si kwa moyo, tulizidi kutamani kwa shauku nyingi kuwaona nyuso zenu. 18 Kwa hiyo tulitaka kuja kwenu, naam, mimi Paulo, mara ya kwanza, na mara ya pili, na Shetani akatuzuia. 19 Maana tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari, ni nini? Je! Si ninyi, mbele za Bwana wetu Yesu, wakati wa kuja kwake? 20 Maana ninyi ndinyi utukufu wetu, na furaha yetu.

1 Wathesalonike 3

1 Basi kwa hiyo, tulipokuwa hatuwezi kuvumilia zaidi, tuliona vema kuachwa Athene peke yetu. 2 Tukamtuma Timotheo ndugu yetu, mtumishi wa Mungu katika Injili ya Kristo, ili kuwafanya ninyi imara na kuwafariji kwa habari ya imani yenu; 3 mtu asifadhaishwe na dhiki hizi; maana ninyi wenyewe mnajua ya kuwa twawekewa hizo. 4 Kwa kuwa tulipokuwapo kwenu tulitangulia kuwaambia kwamba tutapata dhiki, kama ilivyotukia, nanyi mwajua. 5 Kwa hiyo mimi nami nilipokuwa siwezi kuvumilia tena, nalituma mtu ili niijue imani yenu, asije yule mjaribu akawajaribu, na taabu yetu ikawa haina faida. 6 Lakini Timotheo alipotujia hivi sasa kutoka kwenu, alituletea habari njema za imani yenu na upendo wenu, na ya kwamba mnatukumbuka vema siku zote; mkitamani kutuona sisi vile vile kama sisi kuwaona ninyi. 7 Kwa sababu hiyo, ndugu, tulifarijiwa kwa habari zenu, katika msiba na dhiki yetu yote, kwa imani yenu. 8 Kwa kuwa sasa twaishi, ikiwa ninyi mnasimama imara katika Bwana. 9 Maana ni shukrani gani tuwezayo kumlipa Mungu kwa ajili yenu, kwa furaha ile yote tunayoifurahia, kwa sababu yenu mbele za Mungu wetu; 10 usiku na mchana tunapoomba kwa juhudi tupate kuwaona nyuso zenu, na kuyatengeneza mapungufu ya imani yenu? 11 Basi Mungu mwenyewe, Baba yetu, na Bwana wetu Yesu, atuongoze njia yetu tufike kwenu. 12 Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu; 13 apate kuifanya imara mioyo yenu iwe bila lawama katika utakatifu mbele za Mungu, Baba yetu, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu pamoja na watakatifu wake wote.

1 Wathesalonike 4

1 Iliyobaki, ndugu, tunakusihini na kuwaonya kwamba mwenende katika Bwana Yesu; kama mlivyopokea kwetu jinsi iwapasavyo kuenenda na kumpendeza Mungu, kama nanyi mnavyoenenda, vivyo hivyo mpate kuzidi sana. 2 Kwa kuwa mnajua ni maagizo gani tuliyowapa kwa Bwana Yesu. 3 Maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati; 4 kila mmoja wenu ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima; 5 si katika hali ya tamaa mbaya, kama Mataifa wasiomjua Mungu. 6 Mtu asimpunje ndugu yake wala kumkosa katika jambo hili; kwa sababu Bwana ndiye alipizaye kisasi cha haya yote; kama tulivyowaambia kwanza, tukashuhudia sana. 7 Maana Mungu hakutuitia uchafu, bali tuwe katika utakaso. 8 Basi yeye anayekataa, hakatai mwanadamu bali Mungu, anayewapa ninyi Roho wake Mtakatifu. 9 Katika habari ya upendano, hamna haja niwaandikie; maana ninyi wenyewe mmefundishwa na Mungu kupendana. 10 Kwa maana mnafanya neno hili kwa ndugu wote walio katika Makedonia yote. Lakini twawasihi, ndugu, mzidi sana. 11 Tena mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza; 12 ili mwenende kwa adabu mbele yao walio nje, wala msiwe na haja ya kitu cho chote. 13 Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. 14 Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. 15 Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. 16 Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. 17 Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele. 18 Basi, farijianeni kwa maneno hayo.

1 Wathesalonike 5

1 Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie. 2 Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. 3 Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa. 4 Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi. 5 Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza. 6 Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe, na kuwa na kiasi. 7 Maana walalao usingizi hulala usiku, pia na walewao hulewa usiku. 8 Lakini sisi tulio wa mchana, tuwe na kiasi, hali tukijivika kifuani imani na upendo, na chapeo yetu iwe tumaini la wokovu. 9 Kwa kuwa Mungu hakutuweka kwa hasira yake, bali tupate wokovu, kwa Bwana wetu Yesu Kristo; 10 ambaye alikufa kwa ajili yetu, ili tuishi pamoja naye, kwamba twakesha au kwamba twalala. 11 Basi, farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake, vile vile kama mnavyofanya. 12 Lakini, ndugu, tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; 13 mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao. Iweni na amani ninyi kwa ninyi. 14 Ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote. 15 Angalieni mtu awaye yote asimlipe mwenziwe mabaya kwa mabaya; bali siku zote lifuateni lililo jema, ninyi kwa ninyi na kwa watu wote. 16 Furahini siku zote; 17 ombeni bila kukoma; 18 shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu. 19 Msimzimishe Roho; 20 msitweze unabii; 21 jaribuni mambo yote; lishikeni lililo jema; 22 jitengeni na ubaya wa kila namna. 23 Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi nafsi zenu na roho zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo. 24 Yeye ni mwaminifu ambaye awaita, naye atafanya. 25 Ndugu, tuombeeni. 26 Wasalimuni ndugu wote kwa busu takatifu. 27 Nawaapisha kwa Bwana, ndugu wote wasomewe waraka huu. 28 Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi.

2 Wathesalonike 1

1 Paulo, na Silwano, na Timotheo, kwa kanisa la Wathesalonike, lililo katika Mungu Baba yetu, na Bwana Yesu Kristo. 2 Neema na iwe kwenu na amani zitokazo kwa Mungu Baba, na kwa Bwana Yesu Kristo. 3 Ndugu, imetupasa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kama ilivyo wajibu, kwa kuwa imani yenu inazidi sana, na upendo wa kila mtu kwenu kwa mwenzake umekuwa mwingi. 4 Hata na sisi wenyewe twaona fahari juu yenu katika makanisa ya Mungu kwa ajili ya saburi yenu, na imani mliyo nayo katika adha zenu zote na dhiki mnazostahimili. 5 Ndiyo ishara hasa ya hukumu iliyo haki ya Mungu, ili mhesabiwe kuwa mwastahili kuuingia ufalme wa Mungu, ambao kwa ajili yake mnateswa. 6 Kwa kuwa ni haki mbele za Mungu kuwalipa mateso wale wawatesao ninyi; 7 na kuwalipa ninyi mteswao raha pamoja na sisi; wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake 8 katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; 9 watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake; 10 yeye atakapokuja ili kutukuzwa katika watakatifu wake, na kustaajabiwa katika wote waliosadiki katika siku ile, (kwa sababu ushuhuda wetu ulisadikiwa kwenu). 11 Kwa hiyo twawaombea ninyi sikuzote, ili Mungu wetu awahesabu kuwa mmekustahili kuitwa kwenu, akatimiza kila haja ya wema na kila kazi ya imani kwa nguvu; 12 jina la Bwana wetu Yesu litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana Yesu Kristo.

2 Wathesalonike 2

1 Basi, ndugu, tunakusihini, kwa habari ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo, na kukusanyika kwetu mbele zake, 2 kwamba msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha kuwapo. 3 Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; maana haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu; 4 yule mpingamizi, ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa; hata yeye mwenyewe kuketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu. 5 Je! Hamkumbuki ya kuwa wakati nilipokuwapo pamoja nanyi naliwaambieni hayo? 6 Na sasa lizuialo mwalijua, yule apate kufunuliwa wakati wake. 7 Maana ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi; lakini yuko azuiaye sasa, hata atakapoondolewa. 8 Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake; 9 yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; 10 na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa. 11 Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya upotevu, wauamini uongo; 12 ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu. 13 Lakini imetupasa sisi kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, ndugu mliopendwa na Bwana, kwa kuwa Mungu amewachagua tangu mwanzo mpate wokovu, katika kutakaswa na Roho, na kuiamini kweli; 14 aliyowaitia ninyi kwa injili yetu, ili kuupata utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo. 15 Basi, ndugu, simameni imara, mkayashike mapokeo mliyofundishwa, ama kwa maneno, ama kwa waraka wetu. 16 Na Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe, na Mungu Baba yetu, aliyetupenda akatupa faraja ya milele na tumaini jema, katika neema, 17 awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema.

2 Wathesalonike 3

1 Hatimaye, ndugu, tuombeeni, neno la Bwana liendelee, na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu; 2 tukaokolewe na watu wasio haki, wabaya; maana si wote walio na imani. 3 Lakini Bwana ni mwaminifu, atakayewafanya imara na kuwalinda na yule mwovu. 4 Nasi tumemtumaini Bwana kwa mambo yenu, kwamba mnayafanya tulivyowaagiza, tena kwamba mtayafanya. 5 Bwana awaongoze mioyo yenu mkapate pendo la Mungu, na saburi ya Kristo. 6 Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu. 7 Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu; 8 wala hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote. 9 Si kwamba hatuna amri, lakini makusudi tufanye nafsi zetu kuwa kielelezo kwenu, mtufuate. 10 Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula. 11 Maana twasikia kwamba wako watu kwenu waendao bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini wanajishughulisha na mambo ya wengine. 12 Basi twawaagiza hao, na kuwaonya katika Bwana Yesu Kristo, watende kazi kwa utulivu na kula chakula chao wenyewe. 13 Lakini ninyi, ndugu, msikate tamaa katika kutenda mema. 14 Na ikiwa mtu awaye yote halishiki neno letu la waraka huu, jihadharini na mtu huyo, wala msizungumze naye, apate kutahayari; 15 lakini msimhesabu kuwa adui, bali mwonyeni kama ndugu. 16 Sasa, Bwana wa amani mwenyewe na awape amani daima kwa njia zote. Bwana awe pamoja nanyi nyote. 17 Salamu zangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Hii ndiyo alama katika kila waraka, ndio mwandiko wangu. 18 Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi nyote.

1 Timotheo 1

1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu, kwa amri ya Mungu Mwokozi wetu na Kristo Yesu, taraja letu; 2 kwa Timotheo, mwanangu hasa katika imani. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu. 3 Kama vile nilivyokusihi ukae Efeso, nilipokuwa nikisafiri kwenda Makedonia, ili uwakataze wengine wasifundishe elimu nyingine; 4 wala wasiangalie hadithi na nasaba zisizo na ukomo, ziletazo maswali wala si madaraka ya Mungu yaliyo katika imani; basi ufanye hivyo. 5 Walakini mwisho wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki. 6 Wengine wakiyakosa hayo wamegeukia maneno ya ubatili; 7 wapenda kuwa waalimu wa sheria, ingawa hawayafahamu wasemayo wala mambo yale wayanenayo kwa uthabiti. 8 Lakini twajua ya kuwa sheria ni njema, kama mtu akiitumia kwa njia iliyo halali; 9 akilifahamu neno hili, ya kuwa sheria haimhusu mtu wa haki, bali waasi, na wasio wataratibu, na makafiri, na wenye dhambi, na wanajisi, na wasiomcha Mungu, na wapigao baba zao, na wapigao mama zao, na wauaji, 10 na wazinifu, na wafiraji, na waibao watu, na waongo, nao waapao kwa uongo; na likiwapo neno lo lote linginelo lisilopatana na mafundisho yenye uzima; 11 kama vile ilivyonenwa katika Habari Njema ya utukufu wa Mungu ahimidiwaye, niliyowekewa amana. 12 Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; 13 ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri, lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani. 14 Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. 15 Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. 16 Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele. 17 Sasa kwa Mfalme wa milele, asiyeweza kuona uharibifu, asiyeonekana, Mungu peke yake, na iwe heshima na utukufu milele na milele. Amina. 18 Mwanangu Timotheo, nakukabidhi agizo hilo liwe akiba, kwa ajili ya maneno ya unabii yaliyotangulia juu yako, ili katika hayo uvipige vile vita vizuri; 19 uwe mwenye imani na dhamiri njema, ambayo wengine wameisukumia mbali, wakaangamia kwa habari ya Imani. 20 Katika hao wamo Himenayo na Iskanda, ambao nimempa Shetani watu hao, ili wafundishwe wasimtukane Mungu.

1 Timotheo 2

1 Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote; 2 kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu. 3 Hili ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu; 4 ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli. 5 Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; 6 ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake. 7 Nami kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa katika imani na kweli. 8 Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano. 9 Vivyo hivyo wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi; si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za thamani; 10 bali kwa matendo mema, kama iwapasavyo wanawake wanaoukiri uchaji wa Mungu. 11 Mwanamke na ajifunze katika utulivu, akitii kwa kila namna. 12 Simpi mwanamke ruhusa ya kufundisha, wala kumtawala mwanamume, bali awe katika utulivu. 13 Kwa maana Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza, na Hawa baadaye. 14 Wala Adamu hakudanganywa, ila mwanamke alidanganywa kabisa akaingia katika hali ya kukosa. 15 Walakini ataokolewa kwa uzazi wake, kama wakidumu katika imani na upendo na utakaso, pamoja na moyo wa kiasi.

1 Timotheo 3

1 Ni neno la kuaminiwa; mtu akitaka kazi ya askofu, atamani kazi njema. 2 Basi imempasa askofu awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi na busara, mtu wa utaratibu, mkaribishaji, ajuaye kufundisha; 3 si mtu wa kuzoelea ulevi, si mpiga watu; bali awe mpole; si mtu wa kujadiliana, wala asiwe mwenye kupenda fedha; 4 mwenye kuisimamia nyumba yake vema, ajuaye kutiisha watoto katika ustahivu; 5 (yaani, mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa la Mungu?) 6 Wala asiwe mtu aliyeongoka karibu, asije akajivuna akaanguka katika hukumu ya Ibilisi. 7 Tena imempasa kushuhudiwa mema na watu walio nje; ili asianguke katika lawama na mtego wa Ibilisi. 8 Vivyo hivyo mashemasi na wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, si watu wa kutumia mvinyo sana,si watu wanaotamani fedha ya aibu. 9 wakiishika siri ya imani katika dhamiri safi. 10 Hawa pia na wajaribiwe kwanza; baadaye waitende kazi ya shemasi, wakiisha kuonekana kuwa hawana hatia. 11 Vivyo hivyo wake zao na wawe wastahivu; si wasingiziaji; watu wa kiasi, waaminifu katika mambo yote. 12 Mashemasi na wawe waume wa mke mmoja, wakiwasimamia watoto wao vizuri, na nyumba zao. 13 Kwa maana watendao vema kazi ya shemasi hujipatia daraja nzuri, na ujasiri mwingi katika imani iliyo katika Kristo Yesu. 14 Nakuandikia hayo nikitaraji kuja kwako hivi karibu. 15 Lakini nikikawia, upate kujua jinsi iwapasavyo watu kuenenda katika nyumba ya Mungu, iliyo kanisa la Mungu aliye hai, nguzo na msingi wa kweli. 16 Na bila shaka siri ya utauwa ni kuu. Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu.

1 Timotheo 4

1 Basi Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; 2 kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe; 3 wakiwazuia watu wasioe, na kuwaamuru wajiepushe na vyakula, ambavyo Mungu aliviumba vipokewe kwa shukrani na walio na imani wenye kuijua hiyo kweli. 4 Kwa maana kila kiumbe cha Mungu ni kizuri, wala hakuna cha kukataliwa, kama kikipokewa kwa shukrani; 5 kwa kuwa kimetakaswa kwa neno la Mungu na kwa kuomba. 6 Uwakumbushe ndugu mambo hayo, nawe utakuwa mtumishi mwema wa Kristo Yesu, na mzoevu wa maneno ya imani, na mafundisho mazuri yale uliyoyafuata. 7 Bali hadithi za kizee, zisizokuwa za dini, uzikatae; nawe ujizoeze kupata utauwa. 8 Kwa maana kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye. 9 Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa; 10 kwa maana twajitaabisha na kujitahidi kwa kusudi hili, kwa sababu tunamtumaini Mungu aliye hai, aliye Mwokozi wa watu wote, hasa wa waaminio. 11 Mambo hayo uyaagize na kuyafundisha. 12 Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi. 13 Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. 14 Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee. 15 Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote. 16 Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.

1 Timotheo 5

1 Mzee usimkemee, bali umwonye kama baba; na vijana kama ndugu; 2 wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote. 3 Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli. 4 Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. 5 Basi yeye aliye mjane kweli kweli, ameachwa peke yake, huyo amemwekea Mungu tumaini lake, naye hudumu katika maombi na sala mchana na usiku. 6 Bali, yeye asiyejizuia nafsi yake amekufa ingawa yu hai. 7 Mambo hayo pia uyaagize, ili wasiwe na lawama. 8 Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini. 9 Mjane asiandikwe isipokuwa umri wake amepata miaka sitini; naye amekuwa mke wa mume mmoja; 10 naye ameshuhudiwa kwa matendo mema; ikiwa amelea watoto, ikiwa amekaribisha wageni, ikiwa amewaosha watakatifu miguu, ikiwa amewasaidia wateswao, ikiwa amefuata kwa bidii kila tendo jema. 11 Bali wajane walio vijana ukatae kuwaandika hao, maana, wakizidiwa na tamaa kinyume cha Kristo, wataka kuolewa; 12 nao wana hukumu kwa kuwa wameiacha imani yao ya kwanza. 13 Tena, pamoja na hayo, hujifunza kuwa wavivu, wakizunguka-zunguka nyumba kwa nyumba; wala si wavivu tu, lakini ni wachongezi na wadadisi, wakinena maneno yasiyowapasa. 14 Basi napenda wajane, ambao si wazee, waolewe, wazae watoto, wawe na madaraka ya nyumbani; ili wasimpe adui nafasi ya kulaumu. 15 Kwa maana wengine wamekwisha kugeuka na kumfuata Shetani. 16 Mwanamke aaminiye, akiwa ana wajane, na awasaidie mwenyewe, Kanisa lisilemewe; ili liwasaidie wale walio wajane kweli kweli. 17 Wazee watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha. 18 Kwa maana andiko lasema, Usimfunge kinywa ng'ombe apurapo nafaka. Na tena, Mtenda kazi astahili ujira wake. 19 Usikubali mashitaka juu ya mzee, ila kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu. 20 Wale wadumuo kutenda dhambi uwakemee mbele ya wote, ili na wengine waogope. 21 Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, na mbele za malaika wateule, uyatende hayo pasipo kuhukumu kwa haraka; usifanye neno lo lote kwa upendeleo. 22 Usimwekee mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi. 23 Tokea sasa usinywe maji tu lakini tumia mvinyo kidogo, kwa ajili ya tumbo lako, na magonjwa yakupatayo mara kwa mara. 24 Dhambi za watu wengine zi dhahiri, zatangulia kwenda hukumuni; wengine dhambi zao zawafuata. 25 Vivyo hivyo matendo yaliyo mazuri ya dhahiri; wala yale yasiyo dhahiri hayawezi kusitirika.

1 Timotheo 6

1 Wo wote walio chini ya kongwa, hali ya utumwa, na wawahesabie bwana zao kuwa wamestahili heshima yote, jina la Mungu lisitukanwe wala mafundisho yetu. 2 Na wale walio na bwana waaminio wasiwadharau kwa kuwa ni ndugu; bali afadhali wawatumikie, kwa sababu hao waishirikio faida ya kazi yao wamekuwa wenye imani na kupendwa. Mambo hayo uyafundishe na kuonya. 3 Mtu awaye yote akifundisha elimu nyingine, wala hayakubali maneno yenye uzima ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala mafundisho yapatanayo na utauwa, 4 amejivuna; wala hafahamu neno lo lote; bali ana wazimu wa kuwazia habari za maswali, na mashindano ya maneno, ambayo katika hayo hutoka husuda, na ugomvi, na matukano, na shuku mbaya; 5 na majadiliano ya watu walioharibika akili zao, walioikosa kweli, huku wakidhani ya kuwa utauwa ni njia ya kupata faida. 6 Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. 7 Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; 8 ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. 9 Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. 10 Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi. 11 Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole. 12 Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele ulioitiwa, ukaungama maungamo mazuri mbele ya mashahidi wengi. 13 Nakuagiza mbele za Mungu anayevihifadhi hai vitu vyote, na mbele za Kristo Yesu, aliyeyaungama maungamo mazuri yale mbele ya Pontio Pilato, 14 kwamba uilinde amri hii pasipo mawaa, pasipo lawama, hata kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo; 15 ambako yeye kwa majira yake atakudhihirisha, yeye aliyehimidiwa, Mwenye uweza peke yake, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana; 16 ambaye yeye peke yake hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa; wala hakuna mwanadamu aliyemwona, wala awezaye kumwona. Heshima na uweza una yeye hata milele. Amina. 17 Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. 18 Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; 19 huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli. 20 Ee Timotheo, ilinde hiyo amana; ujiepushe na maneno yasiyo ya dini, yasiyo na maana, na mashindano ya elimu iitwayo elimu kwa uongo; 21 ambayo wengine wakiikiri hiyo wameikosa Imani. Neema na iwe pamoja nanyi.

2 Timothy 1

1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu, kwa mapenzi ya Mungu; kwa ajili ya ahadi ya uzima ulio katika Kristo Yesu; 2 kwa Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu. 3 Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana. 4 Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha; 5 nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo. 6 Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. 7 Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi. 8 Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; 9 ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele, 10 na sasa inadhihirishwa kwa kufunuliwa kwake Mwokozi wetu Kristo Yesu; aliyebatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili; 11 ambayo kwa ajili ya hiyo naliwekwa niwe mhubiri na mtume na mwalimu. 12 Kwa sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile. 13 Shika kielelezo cha maneno yenye uzima uliyoyasikia kwangu, katika imani na upendo ulio katika Kristo Yesu. 14 Ilinde ile amana nzuri kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu. 15 Waijua habari hii, ya kuwa wote walio wa Asia waliniepuka, ambao miongoni mwao wamo Figelo na Hermogene. 16 Bwana awape rehema wale walio wa mlango wake Onesiforo; maana mara nyingi aliniburudisha, wala hakuuonea haya mnyororo wangu; 17 bali, alipokuwapo hapa Rumi, alinitafuta kwa bidii akanipata. 18 Bwana na ampe kuona rehema machoni pa Bwana siku ile. Na jinsi alivyonihudumia kwa mengi huko Efeso, wewe unajua sana.

2 Timothy 2

1 Basi wewe, mwanangu, uwe hodari katika neema iliyo katika Kristo Yesu. 2 Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine. 3 Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu. 4 Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari. 5 Hata mtu akishindana katika machezo hapewi taji, asiposhindana kwa halali. 6 Yampasa mkulima mwenye taabu ya kazi kuwa wa kwanza wa kupata fungu la matunda. 7 Yafahamu sana hayo nisemayo, kwa maana Bwana atakupa akili katika mambo yote. 8 Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. 9 Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi. 10 Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele. 11 Ni neno la kuaminiwa. Kwa maana, Kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia; 12 Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi; 13 Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe. 14 Uwakumbushe mambo hayo, ukiwaonya machoni pa Mungu, wasiwe na mashindano ya maneno, ambayo hayana faida, bali huwaharibu wasikiao. 15 Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli. 16 Jiepushe na maneno yasiyo na maana, ambayo si ya dini; kwa kuwa wataendelea zaidi katika maovu, 17 na neno lao litaenea kama donda-ndugu. Miongoni mwa hao wamo Himenayo na Fileto, 18 walioikosa ile kweli, wakisema ya kwamba kiyama imekwisha kuwapo, hata kuipindua imani ya watu kadha wa kadha. 19 Lakini msingi wa Mungu ulio imara umesimama, wenye muhuri hii, Bwana awajua walio wake. Na tena, Kila alitajaye jina la Bwana na auache uovu. 20 Basi katika nyumba kubwa havimo vyombo vya dhahabu na fedha tu, bali na vya mti, na vya udongo; vingine vina heshima, vingine havina. 21 Basi ikiwa mtu amejitakasa kwa kujitenga na hao, atakuwa chombo cha kupata heshima, kilichosafishwa, kimfaacho Bwana, kimetengenezwa kwa kila kazi iliyo njema. 22 Lakini zikimbie tamaa za ujanani; ukafuate haki, na imani, na upendo, na amani, pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi. 23 Walakini uyakatae maswali ya upumbavu yasiyo na elimu, ukijua ya kuwa huzaa magomvi. 24 Tena haimpasi mtumwa wa Bwana kuwa mgomvi; bali kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu; 25 akiwaonya kwa upole wao washindanao naye, ili kama ikiwezekana, Mungu awape kutubu na kuijua kweli; 26 wapate tena fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye, hata kuyafanya mapenzi yake.

2 Timothy 3

1 Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. 2 Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, 3 wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, 4 wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; 5 wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao. 6 Kwa maana katika hao wamo wale wajiingizao katika nyumba za watu, na kuchukua mateka wanawake wajinga wenye mizigo ya dhambi, waliochukuliwa na tamaa za namna nyingi; 7 wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli. 8 Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani. 9 Lakini hawataendelea sana; maana upumbavu wao utakuwa dhahiri kwa watu wote, kama vile na upumbavu wa hao ulivyokuwa dhahiri. 10 Bali wewe umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu, 11 na upendo, na saburi; tena na adha zangu na mateso, mambo yaliyonipata katika Antiokia, katika Ikonio, na katika Listra, kila namna ya adha niliyoistahimili, naye Bwana aliniokoa katika hayo yote. 12 Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa. 13 lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. 14 Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; 15 na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. 16 Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; 17 ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.

2 Timothy 4

1 Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake; 2 lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho. 3 Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; 4 nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo. 5 Bali wewe, uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako. 6 Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika. 7 Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda; 8 baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake. 9 Jitahidi kuja kwangu upesi. 10 Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia. 11 Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi. 12 Lakini Tikiko nalimpeleka Efeso. 13 Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu, hasa vile vya ngozi. 14 Iskanda, mfua shaba, alionyesha ubaya mwingi kwangu; Bwana atamlipa sawasawa na matendo yake. 15 Nawe ujihadhari na huyo, kwa sababu aliyapinga sana maneno yetu. 16 Katika jawabu langu la kwanza hakuna mtu aliyesimama upande wangu, bali wote waliniacha; naomba wasihesabiwe hatia kwa jambo hilo. 17 Lakini Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie Mataifa yote; nami nikaokolewa katika kinywa cha simba. 18 Bwana ataniokoa na kila neno baya, na kunihifadhi hata nifike ufalme wake wa mbinguni. Utukufu una Yeye milele na milele. Amina. 19 Nisalimie Priska na Akila, na wale wa nyumbani mwa Onesiforo. 20 Erasto alikaa Korintho. Trofimo nalimwacha huko Mileto, hawezi. 21 Jitahidi kuja kabla ya wakati wa baridi. Eubulo akusalimu, na Pude, na Lino, na Klaudia, na ndugu wote pia. 22 Bwana na awe pamoja na roho yako. Neema na iwe pamoja nanyi.

Tito 1

1 Paulo, mtumwa wa Mungu, na mtume wa Yesu Kristo; kwa ajili ya imani ya wateule wa Mungu, na ujuzi wa kweli ile iletayo utauwa; 2 katika tumaini la uzima wa milele, ambao Mungu asiyeweza kusema uongo aliuahidi tangu milele; 3 akalifunua neno lake kwa majira yake katika ule ujumbe niliowekewa amana mimi kwa amri ya Mwokozi wetu Mungu; 4 kwa Tito, mwanangu hasa katika imani tuishirikiyo. Neema na iwe kwako na amani zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu. 5 Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji kama vile nilivyokuamuru; 6 ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii. 7 Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno,kwa kuwa ni wakili wa MUNGU;asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake,asiwe mwepesi wa hasira,asiwe mlevi wala mgomvi,asiwe mpenda mapato ya aibu. 8 bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake; 9 akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga. 10 Kwa maana kuna wengi wasiotii, wenye maneno yasiyo na maana, wadanganyaji, na hasa wale wa tohara, ambao yapasa wazibwe vinywa vyao. 11 Hao wanapindua watu wa nyumba nzima, wakifundisha yasiyowapasa kwa ajili ya mapato ya aibu. 12 Mtu wa kwao, nabii wao wenyewe, amesema, Wakrete ni waongo siku zote, hayawani wabaya, walafi wavivu. 13 Ushuhuda huo ni kweli. Kwa sababu hiyo uwakemee kwa ukali, ili wapate kuwa wazima katika imani; 14 wasisikilize hadithi za Kiyahudi, wala maagizo ya watu wajiepushao na yaliyo kweli. 15 Vitu vyote ni safi kwa hao walio safi; lakini hakuna kilicho safi kwao walio wanajisi, wasioamini; bali akili zao zimekuwa najisi, na nia zao pia. 16 Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana; ni wenye machukizo, waasi, wala kwa kila tendo jema hawafai.

Tito 2

1 Lakini wewe nena mambo yapasayo mafundisho yenye uzima; 2 ya kwamba wazee wawe wenye kiasi, wastahivu, wenye busara, wazima katika imani na katika upendo na katika saburi. 3 Vivyo hivyo na wazee wa kike wawe na mwenendo wa utakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye kutumia mvinyo nyingi, bali wafundishao mema; 4 ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; 5 na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe. 6 Vivyo hivyo na vijana waume uwaonye kuwa na kiasi; 7 katika mambo yote ukijionyesha wewe mwenyewe kuwa kielelezo cha matendo mema, na katika mafundisho yako ukionyesha usahihi na ustahivu, 8 na maneno yenye uzima yasiyoweza kuhukumiwa makosa, ili yule mwenye kupinga atahayarike, kwa kuwa hana neno baya la kunena juu yetu. 9 Watumwa na wawatii bwana zao, wakiwapendeza katika mambo yote; wasiwe wenye kujibu, 10 wasiwe waibaji; bali wauonyeshe uaminifu mwema wote, ili wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote. 11 Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; 12 nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa; 13 tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu; 14 ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema. 15 Nena maneno hayo, onya na kukaripia kwa mamlaka yote; asikudharau mtu awaye yote.

Tito 3

1 Uwakumbushe watu kunyenyekea kwa wenye uwezo na mamlaka, na kutii, na kuwa tayari kwa kila kazi njema; 2 wasimtukane mtu ye yote, wasiwe wagomvi, wawe wema, wakionyesha upole wote kwa watu wote. 3 Maana hapo zamani sisi nasi tulikuwa hatuna akili, tulikuwa waasi, tumedanganywa, huku tukitumikia tamaa na anasa za namna nyingi, tukiishi katika uovu na husuda, tukichukiza na kuchukiana. 4 Lakini wema wake Mwokozi wetu Mungu, na upendo wake kwa wanadamu, ulipofunuliwa, alituokoa; 5 si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu; 6 ambaye alitumwagia kwa wingi, kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi wetu; 7 ili tukihesabiwa haki kwa neema yake, tupate kufanywa warithi wa uzima wa milele, kama lilivyo tumaini letu. 8 Ni neno la kuaminiwa; na mambo hayo nataka uyanene kwa nguvu, ili wale waliomwamini Mungu wakumbuke kudumu katika matendo mema. Hayo ni mazuri, tena yana faida kwa wanadamu. 9 Lakini maswali ya upuzi ujiepushe nayo, na nasaba, na magomvi, na mashindano ya sheria. Kwa kuwa hayana faida, tena hayana maana. 10 Mtu aliye mzushi, baada ya kumwonya mara ya kwanza na mara ya pili, mkatae; 11 ukijua ya kuwa mtu kama huyo amepotoka, tena atenda dhambi, maana amejihukumu hatia yeye mwenyewe. 12 Wakati nitakapomtuma Artema kwako au Tikiko, jitahidi kuja kwangu huku Nikopoli; kwa maana huku nimekusudia kukaa wakati wa baridi. 13 Zena, yule mwana-sheria, na Apolo, uwasafirishe kwa bidii, wasipungukiwe na cho chote. 14 Watu wetu nao wajifunze kudumu katika matendo mema, kwa matumizi yaliyo lazima, ili wasiwe hawana matunda. 15 Watu wote walio pamoja nami wakusalimu. Tusalimie wale watupendao katika imani. Neema na iwe pamoja nanyi nyote.

Filemoni 1

1 Paulo, mfungwa wa Kristo Yesu, na Timotheo aliye ndugu yetu, kwa Filemoni mpendwa wetu, mtenda kazi pamoja nasi, 2 na kwa Afia, ndugu yetu, na kwa Arkipo askari mwenzetu, na kwa kanisa lililo katika nyumba yako. 3 Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu, Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo. 4 Namshukuru Mungu wangu sikuzote, nikikukumbuka katika maombi yangu; 5 nikisikia habari za upendo wako na imani uliyo nayo kwa Bwana Yesu na kwa watakatifu wote; 6 ili kwamba ushirika wa imani yako ufanye kazi yake, katika ujuzi wa kila kitu chema kilicho kwetu, katika Kristo. 7 Maana nalikuwa na furaha nyingi na faraja kwa sababu ya upendo wako, kwa kuwa mioyo ya watakatifu imeburudishwa nawe, ndugu yangu. 8 Kwa hiyo, nijapokuwa nina ujasiri katika Kristo kukuagiza likupasalo; 9 lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia. 10 Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; 11 ambaye zamani alikuwa hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; 12 niliyemtuma kwako, yeye mwenyewe, maana ni moyo wangu hasa; 13 ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili. 14 Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari. 15 Maana, labda ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele; 16 tokea sasa, si kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana. 17 Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe. 18 Na kama amekudhulumu, au unamwia kitu, ukiandike hicho juu yangu. 19 Mimi Paulo nimeandika kwa mkono wangu mwenyewe, mimi nitalipa. Sikuambii kwamba nakuwia hata nafsi yako. 20 Naam, ndugu yangu, nipate faida kwako katika Bwana; uniburudishe moyo wangu katika Kristo. 21 Kwa kuwa nakuamini kutii kwako ndiyo maana nimekuandikia, nikijua ya kuwa utafanya zaidi ya hayo nisemayo. 22 Na pamoja na hayo uniwekee tayari mahali pa kukaa; maana nataraji ya kwamba kwa maombi yenu mtajaliwa kunipata. 23 Epafra, aliyefungwa pamoja nami katika Kristo Yesu, akusalimu; 24 na Marko, na Aristarko, na Dema, na Luka, watendao kazi pamoja nami. 25 Neema ya Bwana Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu.

Waebrania 1

1 Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, 2 mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu. 3 Yeye kwa kuwa ni mng'ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake, akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu; 4 amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao. 5 Kwa maana alimwambia malaika yupi wakati wo wote, Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa? Na tena, Mimi nitakuwa kwake baba, Na yeye atakuwa kwangu mwana? 6 Hata tena, amletapo mzaliwa wa kwanza ulimwenguni, asema, Na wamsujudu malaika wote wa Mungu. 7 Na kwa habari za malaika asema, Afanyaye malaika zake kuwa pepo, Na watumishi wake kuwa miali ya moto. 8 Lakini kwa habari za Mwana asema, Kiti chako cha enzi,Mungu,ni cha milele na milele; Na fimbo ya ufalme wako ni fimbo ya adili. 9 Umependa haki, umechukia maasi; Kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta, Mafuta ya shangwe kupita wenzio. 10 Na tena, Wewe,Bwana,hapo mwanzo uliitia misingi ya nchi, Na mbingu ni kazi za mikono yako; 11 Hizo zitaharibika, bali wewe unadumu; Nazo zote zitachakaa kama nguo, 12 Na kama mavazi utazizinga, nazo zitabadilika; Lakini wewe u yeye yule, Na miaka yako haitakoma. 13 Je! Yuko malaika aliyemwambia wakati wo wote, Uketi mkono wangu wa kuume Hata nitakapoweka adui zako chini ya nyayo zako? 14 Je! Hao wote si roho watumikao, wakitumwa kuwahudumu wale watakaourithi wokovu?

Waebrania 2

1 Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa. 2 Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, 3 sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia; 4 Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe. 5 Maana hakuuweka chini ya malaika ulimwengu ule ujao tunaounena, ila mtu mmoja ameshuhudia hivi mahali fulani, akisema, 6 Mwanadamu ni nini hata umkumbuke, Ama mwana wa binadamu, hata umwangalie? 7 Umemfanya mdogo punde kuliko malaika, Umemvika taji ya utukufu na heshima, Umemtawaza juu ya kazi za mikono yako; 8 Umeweka vitu vyote chini ya nyayo zake. Kwa maana katika kuweka vitu vyote chini yake hakusaza kitu kisichowekwa chini yake. Lakini sasa bado hatujaona vitu vyote kutiwa chini yake. 9 ila twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu. 10 Kwa kuwa ilimpasa yeye, ambaye kwa ajili yake na kwa njia yake vitu vyote vimekuwapo, akileta wana wengi waufikilie utukufu, kumkamilisha kiongozi mkuu wa wokovu wao kwa njia ya mateso. 11 Maana yeye atakasaye na hao wanaotakaswa wote pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake; 12 akisema, Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu; Katikati ya kanisa nitakuimbia sifa. 13 Na tena, Nitakuwa nimemtumaini yeye. Na tena, Tazama,mimi nipo hapa na watoto niliopewa na Mungu. 14 Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi, 15 awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa. 16 Maana ni hakika, hatwai asili ya malaika, ila atwaa asili ya mzao wa Ibrahimu. 17 Hivyo ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake. 18 Na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.

Waebrania 3

1 Kwa hiyo, ndugu watakatifu, wenye kuushiriki mwito wa mbinguni, mtafakarini sana Mtume na Kuhani Mkuu wa maungamo yetu, Yesu, 2 aliyekuwa mwaminifu kwake yeye aliyemweka, kama Musa naye alivyokuwa, katika nyumba yote ya Mungu. 3 Kwa maana huyo amehesabiwa kuwa amestahili utukufu zaidi kuliko Musa, kama vile yeye aitengenezaye nyumba alivyo na heshima zaidi ya hiyo nyumba. 4 Maana kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu. 5 Na Musa kweli alikuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu kama mtumishi, awe ushuhuda wa mambo yatakayonenwa baadaye; 6 bali Kristo, kama mwana, juu ya nyumba ya Mungu; ambaye nyumba yake ni sisi, kama tukishikamana sana na ujasiri wetu na fahari ya taraja letu mpaka mwisho. 7 Kwa hiyo, kama anenavyo Roho Mtakatifu, Leo, kama mtaisikia sauti yake, 8 Msifanye migumu mioyo yenu, Kama wakati wa kukasirisha, Siku ya kujaribiwa katika jangwa, 9 Hapo baba zenu waliponijaribu, wakanipima, Wakaona matendo yangu miaka arobaini. 10 Kwa hiyo nalichukizwa na kizazi hiki, Nikasema, Sikuzote ni watu waliopotoka mioyo hawa; Hawakuzijua njia zangu; 11 Kama nilivyoapa kwa hasira yangu, Hawataingia rahani mwangu. 12 Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai. 13 Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi. 14 Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho; 15 hapo inenwapo, Leo, kama mtaisikia sauti yake, Msifanye migumu mioyo yenu, Kama wakati wa kukasirisha. 16 Maana ni akina nani waliokasirisha, waliposikia? Si wale wote waliotoka Misri wakiongozwa na Musa? 17 Tena ni akina nani aliochukizwa nao miaka arobaini? Si wale waliokosa, ambao mizoga yao ilianguka katika jangwa? 18 Tena ni akina nani aliowaapia ya kwamba hawataingia katika raha yake, ila wale walioasi? 19 Basi twaona ya kuwa hawakuweza kuingia kwa sababu ya kutokuamini kwao.

Waebrania 4

1 Basi, ikiwa ikaliko ahadi ya kuingia katika raha yake, na tuogope, mmoja wenu asije akaonekana ameikosa. 2 Maana ni kweli, sisi nasi tumehubiriwa habari njema vile vile kama hao. Lakini neno lile lililosikiwa halikuwafaa hao, kwa sababu halikuchanganyika na imani ndani yao waliosikia. 3 Maana sisi tulioamini tunaingia katika raha ile; kama vile alivyosema, Kama nilivyoapa kwa hasira yangu, Hawataingia rahani mwangu: 4 Kwa maana ameinena siku ya saba mahali fulani hivi, Mungu alistarehe siku ya saba, akaziacha kazi zake zote; 5 na hapa napo, Hawataingia rahani mwangu. 6 Basi, kwa kuwa neno hili limebaki kwamba wako watu watakaoingia humo, na wale waliohubiriwa habari ile zamani walikosa kuingia kwa sababu ya kuasi kwao, 7 aweka tena siku fulani, akisema katika Daudi baada ya muda mwingi namna hii, Leo; kama ilivyonenwa tangu zamani, Leo,kama mtaisikia sauti yake, Msifanye migumu mioyo yenu. 8 Maana kama Yoshua angaliwapa raha, asingaliinena siku nyingine baadaye. 9 Basi, imesalia raha ya sabato kwa watu wa Mungu. 10 Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake. 11 Basi, na tufanye bidii kuingia katika raha ile, ili kwamba mtu ye yote asije akaanguka kwa mfano uo huo wa kuasi. 12 Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo. 13 Wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu. 14 Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. 15 Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. 16 Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.

Waebrania 5

1 Maana kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi; 2 awezaye kuwachukulia kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea, kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali ya udhaifu; 3 na kwa sababu hiyo imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi. 4 Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu, kama vile Haruni. 5 Vivyo hivyo Kristo naye hakujitukuza nafsi yake kufanywa kuhani mkuu, lakini yeye aliyemwambia, Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa. 6 kama asemavyo mahali pengine, Ndiwe kuhani wa milele Kwa mfano wa Melkizedeki. 7 Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; 8 na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; 9 naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii; 10 kisha ametajwa na Mungu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki. 11 Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. 12 Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. 13 Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. 14 Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.

Waebrania 6

1 Kwa sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundisho ya kwanza ya Kristo, tukaze mwendo ili tuufikilie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na uhai, na wa kuwa na imani kwa Mungu, 2 na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea mikono, na kufufuliwa wafu, na hukumu ya milele. 3 Na hayo tutafanya Mungu akitujalia. 4 Kwa maana hao waliokwisha kupewa nuru, na kukionja kipawa cha mbinguni, na kufanywa washirika wa Roho Mtakatifu, 5 na kulionja neno zuri la Mungu, na nguvu za zamani zijazo, 6 wakaanguka baada ya hayo, haiwezekani kuwafanya upya tena hata wakatubu; kwa kuwa wamsulibisha Mwana wa Mungu mara ya pili kwa nafsi zao, na kumfedhehi kwa dhahiri. 7 Maana nchi inayoinywa mvua inayoinyeshea mara kwa mara, na kuzaa mboga zenye manufaa kwa hao ambao kwa ajili yao yalimwa, hushiriki baraka zitokazo kwa Mungu; 8 bali ikitoa miiba na magugu hukataliwa na kuwa karibu na laana; ambayo mwisho wake ni kuteketezwa. 9 Lakini, wapenzi, ijapokuwa twanena hayo, katika habari zenu tumesadiki mambo yaliyo mazuri zaidi, na yaliyo na wokovu. 10 Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia. 11 Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; 12 ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu. 13 Kwa maana Mungu, alipompa Ibrahimu ahadi, kwa sababu alikuwa hana mkubwa kuliko yeye mwenyewe wa kumwapa, aliapa kwa nafsi yake, 14 akisema, Hakika yangu kubariki nitakubariki, na kuongeza nitakuongeza. 15 Na hivyo kwa kuvumilia akaipata ile ahadi. 16 Maana wanadamu huapa kwa yeye aliye mkuu kuliko wao; na kwao ukomo wa mashindano yote ya maneno ni kiapo, kwa kuyathibitisha. 17 Katika neno hilo Mungu, akitaka kuwaonyesha zaidi sana warithio ile ahadi, jinsi mashauri yake yasivyoweza kubadilika, alitia kiapo katikati; 18 ili kwa vitu viwili visivyoweza kubadilika, ambavyo katika hivyo Mungu hawezi kusema uongo, tupate faraja iliyo imara, sisi tuliokimbilia kuyashika matumaini yale yawekwayo mbele yetu; 19 tuliyo nayo kama nanga ya roho, yenye salama, yenye nguvu, yaingiayo hata mle mlimo ndani ya pazia, 20 alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu, amekuwa kuhani mkuu hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.

Waebrania 7

1 Kwa maana Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwapiga hao wafalme, akambariki; 2 ambaye Ibrahimu alimgawia sehemu ya kumi ya vitu vyote; (tafsiri ya jina lake kwanza ni mfalme wa haki, tena, mfalme wa Salemu, maana yake, mfalme wa amani; 3 hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake, bali amefananishwa na Mwana wa Mungu); huyo adumu kuhani milele. 4 Basi, angalieni jinsi mtu huyo alivyokuwa mkuu, ambaye Ibrahimu, baba yetu mkuu, alimpa sehemu ya kumi ya nyara. 5 Na katika wana wa Lawi nao, wale waupatao ukuhani, wana amri kutwaa sehemu ya kumi kwa watu wao, yaani, ndugu zao, kwa agizo la sheria, ijapokuwa wametoka katika viuno vya Ibrahimu. 6 Bali yeye, ambaye uzazi wake haukuhesabiwa kuwa umetoka kwa hao, alitwaa sehemu ya kumi kwa Ibrahimu, akambariki yeye aliye na ile ahadi. 7 Wala haikanushiki kabisa kwamba mdogo hubarikiwa na mkubwa. 8 Na hapa wanadamu wapatikanao na kufa hutwaa sehemu ya kumi; bali huko yeye ashuhudiwaye kwamba yu hai. 9 Tena yaweza kusemwa ya kuwa, kwa njia ya Ibrahimu, hata Lawi apokeaye sehemu ya kumi alitoa sehemu ya kumi; 10 kwa maana alikuwa katika viuno vya baba yake, hapo Melkizedeki alipokutana naye. 11 Basi, kama ukamilifu ulikuwapo kwa ukuhani wa Lawi; (maana watu wale waliipata sheria kwa huo); kulikuwa na haja gani tena ya kuhani mwingine ainuke, kwa mfano wa Melkizedeki, wala asihesabiwe kwa mfano wa Haruni? 12 Maana ukuhani ule ukibadilika, hapana budi sheria nayo ibadilike. 13 Maana yeye aliyenenwa hayo alikuwa mshirika wa kabila nyingine, ambayo hapana mtu wa kabila hiyo aliyeihudumia madhabahu. 14 Maana ni dhahiri kwamba Bwana wetu alitoka katika Yuda, kabila ambayo Musa hakunena neno lo lote juu yake katika mambo ya ukuhani. 15 Tena hayo tusemayo ni dhahiri sana zaidi, ikiwa ametokea kuhani mwingine mithili ya Melkizedeki; 16 asiyekuwa kuhani kwa sheria ya amri iliyo ya jinsi ya mwili, bali kwa nguvu za uzima usio na ukomo; 17 maana ameshuhudiwa kwamba, Wewe u kuhani milele Kwa mfano wa Melkizedeki. 18 Maana, kuna kubatiliwa kwa ile amri iliyotangulia, kwa sababu ya udhaifu wake, na kutokufaa kwake; 19 (kwa maana ile sheria haikukamilisha neno); na pamoja na hayo kuliingizwa matumaini yaliyo mazuri zaidi, ambayo kwa hayo twamkaribia Mungu. 20 Na kwa kuwa haikuwa pasipo kiapo, 21 (maana wale walifanywa makuhani pasipo kiapo; bali yeye, pamoja na kiapo, kwa yeye aliyemwambia, Bwana ameapa wala hataghairi, Wewe u kuhani wa milele;) 22 basi kwa kadiri hii Yesu amekuwa mdhamini wa agano lililo bora zaidi. 23 Tena wale walifanywa makuhani wengi, kwa sababu wazuiliwa na mauti wasikae; 24 bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. 25 Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee. 26 Maana ilitupasa sisi tuwe na kuhani mkuu wa namna hii aliye mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko mbingu; 27 ambaye hana haja kila siku, mfano wa wale makuhani wakuu wengine, kwanza kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe, kisha kwa ajili ya dhambi za hao watu; maana yeye alifanya hivi mara moja, alipojitoa nafsi yake. 28 Maana torati yawaweka wanadamu walio na unyonge kuwa makuhani wakuu; bali hilo neno la kiapo kilichokuja baada ya torati limemweka Mwana, aliyekamilika hata milele.

Waebrania 8

1 Basi, katika hayo tunayosema, neno lililo kuu ndilo hili: Tunaye kuhani mkuu wa namna hii, aliyeketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Ukuu mbinguni, 2 mhudumu wa patakatifu, na wa ile hema ya kweli, ambayo Bwana aliiweka wala si mwanadamu. 3 Maana kila kuhani mkuu huwekwa ili atoe vipawa na dhabihu; kwa hiyo lazima huyu naye awe na kitu cha kutoa. 4 Kama angekuwa juu ya nchi, asingekuwa kuhani; maana wako watoao sadaka kama iagizavyo sheria; 5 watumikiao mfano na kivuli cha mambo ya mbinguni, kama Musa alivyoagizwa na Mungu, alipokuwa tayari kuifanya ile hema; maana asema, Angalia ukavifanye vitu vyote kwa mfano ule ulioonyeshwa katika mlima. 6 Lakini sasa amepata huduma iliyo bora zaidi, kwa kadiri alivyo mjumbe wa agano lililo bora, lililoamriwa juu ya ahadi zilizo bora. 7 Maana kama lile la kwanza lingalikuwa halina upungufu, nafasi isingalitafutwa kwa lile la pili. 8 Maana, awalaumupo, asema Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, Nami nitawatimizia nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda agano jipya; 9 Halitakuwa kama agano lile nililoagana na baba zao, Katika siku ile nilipowashika mikono yao niwatoe katika nchi ya Misri. Kwa sababu hawakudumu katika agano langu, Mimi nami sikuwajali asema Bwana. 10 Maana hili ndilo agano nitakaloagana na nyumba ya Israeli Baada ya siku zile, asema Bwana; Nitawapa sheria zangu katika nia zao, Na katika mioyo yao nitaziandika; Nami nitakuwa Mungu kwao, Nao watakuwa watu wangu. 11 Nao hawatafundishana kila mtu na jirani yake, Na kila mtu na ndugu yake, akisema, Mjue Bwana; Kwa maana wote watanijua, Tangu mdogo wao hata mkubwa wao. 12 Kwa sababu nitawasamehe maovu yao, Na dhambi zao sitazikumbuka tena. 13 Kwa kule kusema, Agano jipya, amelifanya lile la kwanza kuwa kuukuu. Lakini kitu kianzacho kuwa kikuukuu na kuchakaa ki karibu na kutoweka.

Waebrania 9

1 Basi hata agano la kwanza lilikuwa na kawaida za ibada, na patakatifu pake, pa kidunia. 2 Maana hema ilitengenezwa, ile ya kwanza, mlimokuwa na kinara cha taa, na meza, na mikate ya Wonyesho; ndipo palipoitwa, Patakatifu. 3 Na nyuma ya pazia la pili, ile hema iitwayo Patakatifu pa patakatifu, 4 yenye chetezo cha dhahabu, na sanduku la agano lililofunikwa kwa dhahabu pande zote, mlimokuwa na kopo la dhahabu lenye ile mana, na ile fimbo ya Haruni iliyochipuka, na vile vibao vya agano; 5 na juu yake makerubi ya utukufu, yakikitia kivuli kiti cha rehema; basi hatuna nafasi sasa ya kueleza habari za vitu hivi kimoja kimoja. 6 Basi, vitu hivi vikiisha kutengenezwa hivyo, makuhani huingia katika hema hiyo ya kwanza daima, wakiyatimiza mambo ya ibada. 7 Lakini katika hema hiyo ya pili kuhani mkuu huingia peke yake, mara moja kila mwaka; wala si pasipo damu, atoayo kwa ajili ya nafsi yake na kwa dhambi za kutokujua za hao watu. 8 Roho Mtakatifu akionyesha neno hili, ya kwamba njia ya kupaingia patakatifu ilikuwa haijadhihirishwa bado, hapo hema ya kwanza ilipokuwa ingali ikisimama; 9 ambayo ndiyo mfano wa wakati huu uliopo sasa; wakati huo sadaka na dhabihu zinatolewa, zisizoweza kwa jinsi ya dhambi kumkamilisha mtu aabuduye, 10 kwa kuwa ni sheria za jinsi ya mwili tu, vyakula na vinywaji na kutawadha kwingine kwingine, zilizoamriwa hata wakati wa matengenezo mapya. 11 Lakini Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa mambo mema yatakayokuwapo, kwa hema iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika kwa mikono, maana yake, isiyo ya ulimwengu huu, 12 wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele. 13 Kwa maana, ikiwa damu ya mbuzi na mafahali na majivu ya ndama ya ng'ombe waliyonyunyiziwa wenye uchafu hutakasa hata kuusafisha mwili; 14 basi si zaidi damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu, mpate kumwabudu Mungu aliye hai? 15 Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele. 16 Maana agano la urithi lilipo, lazima iwepo mauti yake aliyelifanya. 17 Kwa maana agano la urithi lina nguvu palipotukia kufa kwa mtu; kwa kuwa halina nguvu kabisa, akiwa yu hai yeye aliyelifanya. 18 Kwa hiyo hata lile la kwanza halikuanzwa pasipo damu. 19 Maana kila amri ilipokwisha kunenwa na Musa kwa hao watu wote, kama ilivyoamuru sheria, aliitwaa damu ya ndama na ya mbuzi, pamoja na maji na sufu nyekundu na hisopo, akakinyunyizia kitabu chenyewe, na watu wote, 20 akisema, Hii ni damu ya agano mliloamriwa na Mungu. 21 Na ile hema nayo na vyombo vyote vya ibada alivinyunyizia damu vivyo hivyo. 22 Na katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo. 23 Basi ilikuwa sharti nakala za mambo yaliyo mbinguni zisafishwe kwa hizo, lakini mambo ya mbinguni yenyewe yasafishwe kwa dhabihu zilizo bora kuliko hizo. 24 Kwa sababu Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu; 25 wala si kwamba ajitoe mara nyingi, kama vile kuhani mkuu aingiavyo katika patakatifu kila mwaka kwa damu isiyo yake; 26 kama ni hivyo, ingalimpasa kuteswa mara nyingi tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu; lakini sasa, mara moja tu, katika utimilifu wa nyakati, amefunuliwa, azitangue dhambi kwa dhabihu ya nafsi yake. 27 Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu; 28 kadhalika Kristo naye, akiisha kutolewa sadaka mara moja azichukue dhambi za watu wengi; atatokea mara ya pili, pasipo dhambi, kwa hao wamtazamiao kwa wokovu.

Waebrania 10

1 Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao. 2 Kama ndivyo, je! Dhabihu hazingekoma kutolewa; kwa maana waabuduo, wakiisha kusafishwa mara moja, wasingejiona tena kuwa na dhambi? 3 Lakini katika dhabihu hizo liko kumbukumbu la dhambi kila mwaka. 4 Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi. 5 Kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema, Dhabihu na toleo hukutaka, Lakini mwili uliniwekea tayari; 6 Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo; 7 Ndipo niliposema, Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) Niyafanye mapenzi yako, Mungu. 8 Hapo juu asemapo, Dhabihu na matoleo na sadaka za kuteketezwa na hizo za dhambi hukuzitaka, wala hukupendezwa nazo (zitolewazo kama ilivyoamuru torati), 9 ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili. 10 Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu. 11 Na kila kuhani husimama kila siku akifanya ibada, na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi; ambazo haziwezi kabisa kuondoa dhambi. 12 Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; 13 tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake. 14 Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa. 15 Na Roho Mtakatifu naye amshuhudia; kwa maana, baada ya kusema, 16 Hili ni agano nitakaloagana nao baada ya siku zile, anena Bwana, Nitatia sheria zangu mioyoni mwao, Na katika nia zao nitaziandika; ndipo anenapo, 17 Dhambi zao na uasi wao sitaukumbuka tena kabisa. 18 Basi, ondoleo la hayo likiwapo, hapana toleo tena kwa ajili ya dhambi. 19 Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, 20 njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; 21 na kuwa na kuhani mkuu juu ya nyumba ya Mungu; 22 na tukaribie wenye moyo wa kweli, kwa utimilifu wa imani, hali tumenyunyiziwa mioyo tuache dhamiri mbaya, tumeoshwa miili kwa maji safi. 23 Na mlishike sana ungamo la tumaini letu, lisigeuke; maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu; 24 tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; 25 wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia. 26 Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; 27 bali kuna kuitazamia hukumu yenye kutisha, na ukali wa moto ulio tayari kuwala wao wapingao. 28 Mtu aliyeidharau sheria ya Musa hufa pasipo huruma, kwa neno la mashahidi wawili au watatu. 29 Mwaonaje? Haikumpasa adhabu iliyo kubwa zaidi mtu yule aliyemkanyaga Mwana wa Mungu, na kuihesabu damu ya agano aliyotakaswa kwayo kuwa ni kitu ovyo, na kumfanyia jeuri Roho wa neema? 30 Maana twamjua yeye aliyesema, Kupatiliza kisasi ni juu yangu, mimi nitalipa. Na tena, Bwana atawahukumu watu wake. 31 Ni jambo la kutisha kuanguka katika mikono ya Mungu aliye hai. 32 Lakini zikumbukeni siku za kwanza, ambazo, mlipokwisha kutiwa nuru, mlistahimili mashindano makubwa ya maumivu; 33 pindi mlipotwezwa kwa mashutumu na dhiki, na pindi mliposhirikiana na wale waliotendewa hayo. 34 Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang'anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo. 35 Basi msiutupe ujasiri wenu, kwa maana una thawabu kuu. 36 Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi. 37 Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, Yeye ajaye atakuja, wala hatakawia. 38 Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye. 39 Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho zetu.

Waebrania 11

1 Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana. 2 Maana kwa hiyo wazee wetu walishuhudiwa. 3 Kwa imani twafahamu ya kuwa ulimwengu uliumbwa kwa neno la Mungu, hata vitu vinavyoonekana havikufanywa kwa vitu vilivyo dhahiri. 4 Kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akazishuhudia sadaka zake, na kwa hiyo, ijapokuwa amekufa, angali akinena. 5 Kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha; maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu. 6 Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao. 7 Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu, aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake. Na hivyo akauhukumu makosa ulimwengu, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa imani. 8 Kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako. 9 Kwa imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake, akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile ile. 10 Maana alikuwa akiutazamia mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu. 11 Kwa imani hata Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba; alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu. 12 Na kwa ajili ya hayo wakazaliwa na mtu mmoja, naye alikuwa kama mfu, watu wengi kama nyota za mbinguni wingi wao, na kama mchanga ulio ufuoni, usioweza kuhesabika. 13 Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi. 14 Maana hao wasemao maneno kama hayo waonyesha wazi kwamba wanatafuta nchi yao wenyewe. 15 Na kama wangaliikumbuka nchi ile waliyotoka, wangalipata nafasi ya kurejea. 16 Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji. 17 Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee; 18 naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa, 19 akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena toka huko kwa mfano. 20 Kwa imani Isaka akawabariki Yakobo na Esau, hata katika habari ya mambo yatakayokuwa baadaye. 21 Kwa imani Yakobo, alipokuwa katika kufa, akambariki kila mmoja wa wana wa Yusufu, akaabudu akiegemea kichwa cha fimbo yake. 22 Kwa imani Yusufu, alipokuwa amekaribia mwisho wake, alitaja habari za kutoka kwao wana wa Israeli, akaagiza kwa habari ya mifupa yake. 23 Kwa imani Musa, alipozaliwa, akafichwa miezi mitatu na wazazi wake, kwa sababu waliona kwamba ni mtoto mzuri; wala hawakuiogopa amri ya mfalme. 24 Kwa imani Musa alipokuwa mtu mzima, akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; 25 akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo; 26 akihesabu ya kuwa kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri; kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo. 27 Kwa imani akatoka Misri, asiogope ghadhabu ya mfalme; maana alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana. 28 Kwa imani akaifanya Pasaka, na kule kunyunyiza damu, ili yule mwenye kuwaangamiza wazaliwa wa kwanza asiwaguse wao. 29 Kwa imani wakapita kati ya Bahari ya Shamu, kama katika nchi kavu; Wamisri walipojaribu kufanya vivyo wakatoswa. 30 Kwa imani kuta za Yeriko zikaanguka, zilipokwisha kuzungukwa siku saba. 31 Kwa imani Rahabu, yule kahaba, hakuangamia pamoja na hao walioasi; kwa kuwa aliwakaribisha wale wapelelezi kwa amani. 32 Nami niseme nini tena? Maana wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; 33 ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, 34 walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni. 35 Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora; 36 wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; 37 walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya; 38 (watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao), walikuwa wakizunguka-zunguka katika nyika na katika milima na katika mapango na katika mashimo ya nchi. 39 Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi; 40 kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi.

Waebrania 12

1 Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, 2 tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. 3 Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu. 4 Hamjafanya vita hata kumwagika damu, mkishindana na dhambi; 5 tena mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana, Wala usizimie moyo ukikemewa naye; 6 Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye. 7 Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? 8 Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. 9 Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? 10 Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake. 11 Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani. 12 Kwa hiyo inyosheni mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, 13 mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe. 14 Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; 15 mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo. 16 Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja. 17 Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), ijapokuwa aliitafuta sana kwa machozi. 18 Maana hamkufikilia mlima uwezao kuguswa, uliowaka moto, wala wingu jeusi, na giza, na tufani, 19 na mlio wa baragumu na sauti ya maneno; ambayo wale walioisikia walisihi wasiambiwe neno lo lote lingine; 20 maana hawakuweza kustahimili neno lile lililoamriwa, Hata mnyama akiugusa huo mlima atapigwa kwa mawe. 21 Na hayo yaliyoonekana jinsi yalivyokuwa ya kutisha, hata Musa akasema, Nimeshikwa na hofu na kutetemeka. 22 Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi, 23 mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika, 24 na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili. 25 Angalieni msimkatae yeye anenaye. Maana ikiwa hawakuokoka wale waliomkataa yeye aliyewaonya juu ya nchi, zaidi sana hatutaokoka sisi tukijiepusha na yeye atuonyaye kutoka mbinguni; 26 ambaye sauti yake iliitetemesha nchi wakati ule; lakini sasa ameahidi akisema, Mara moja tena nitatetemesha si nchi tu, bali na mbingu pia. 27 Lakini neno lile, Mara moja tena, ladhihirisha kuhamishwa vile viwezavyo kutetemeshwa, kama vitu vilivyoumbwa, vitu visivyoweza kutetemeshwa vikae. 28 Basi kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na mwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho; 29 maana Mungu wetu ni moto ulao.

Waebrania 13

1 Upendano wa ndugu na udumu. 2 Msisahau kuwafadhili wageni; maana kwa njia hii wengine wamewakaribisha malaika pasipo kujua. 3 Wakumbukeni hao waliofungwa kana kwamba mmefungwa pamoja nao; na hao wanaodhulumiwa, kwa vile ninyi nanyi mlivyo katika mwili. 4 Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu. 5 Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. 6 Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? 7 Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao. 8 Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele. 9 Msichukuliwe na mafundisho ya namna nyingine nyingine, na ya kigeni; maana ni vizuri moyo ufanywe imara kwa neema, wala si kwa vyakula, ambavyo wao waliokwenda navyo hawakupata faida. 10 Tuna madhabahu ambayo wale waihudumiao ile hema hawana ruhusa kula vitu vyake. 11 Maana wanyama wale ambao damu yao huletwa ndani ya patakatifu na kuhani mkuu kwa ajili ya dhambi, viwiliwili vyao huteketezwa nje ya kambi. 12 Kwa ajili hii Yesu naye, ili awatakase watu kwa damu yake mwenyewe, aliteswa nje ya lango. 13 Basi na tutoke tumwendee nje ya kambi, tukichukua shutumu lake. 14 Maana hapa hatuna mji udumuo, bali twautafuta ule ujao. 15 Basi, kwa njia yake yeye, na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake. 16 Lakini msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizi ndizo zimpendezazo Mungu. 17 Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi. 18 Tuombeeni; maana tunaamini kwamba tuna dhamiri njema, tukitaka kuwa na mwenendo mwema katika mambo yote. 19 Nami nawasihi zaidi sana kufanya hayo ili nirudishwe kwenu upesi. 20 Basi, Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu Mchungaji Mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu Yesu, 21 awafanye ninyi kuwa wakamilifu katika kila tendo jema, mpate kuyafanya mapenzi yake, naye akifanya ndani yetu lipendezalo mbele zake, kwa Yesu Kristo; utukufu una yeye milele na milele. Amina. 22 Lakini nawasihi, ndugu, mchukuliane na neno hili lenye maonyo maana nimewaandikia kwa maneno machache. 23 Jueni ya kuwa ndugu yetu Timotheo amekwisha kufunguliwa; ambaye, akija upesi, nitaonana nanyi pamoja naye. 24 Wasalimuni wote wenye kuwaongoza, na watakatifu wote; hao walio wa Italia wanawasalimu. 25 Neema na iwe nanyi nyote.

Yakobo 1

1 Yakobo, mtumwa wa Mungu, na wa Bwana Yesu Kristo, kwa kabila kumi na mbili waliotawanyika; salamu. 2 Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; 3 mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. 4 Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno. 5 Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. 6 Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. 7 Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana. 8 Mtu wa nia mbili husita-sita katika njia zake zote. 9 Lakini ndugu asiye na cheo na afurahi kwa kuwa ametukuzwa; 10 bali tajiri kwa kuwa ameshushwa; kwa maana kama ua la majani atatoweka. 11 Maana jua huchomoza kwa hari, huyakausha majani; ua lake huanguka, uzuri wa umbo lake hupotea; vivyo hivyo naye tajiri atanyauka katika njia zake. 12 Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao. 13 Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu. 14 Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. 15 Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti. 16 Ndugu zangu wapenzi, msidanganyike. 17 Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka. 18 Kwa kupenda kwake mwenyewe alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake. 19 Hayo mnajua, ndugu zangu wapenzi. Basi kila mtu na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema; wala kukasirika; 20 kwa maana hasira ya mwanadamu haiitendi haki ya Mungu. 21 Kwa hiyo wekeeni mbali uchafu wote na ubaya uzidio, na kupokea kwa upole neno lile lililopandwa ndani, liwezalo kuziokoa roho zenu. 22 Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. 23 Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. 24 Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo. 25 Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake. 26 Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai. 27 Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.

Yakobo 2

1 Ndugu zangu, imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, Bwana wa utukufu, msiwe nayo kwa kupendelea watu. 2 Maana akiingia katika sinagogi lenu mtu mwenye pete ya dhahabu na mavazi mazuri; kisha akiingia na maskini, mwenye mavazi mabovu; 3 nanyi mkimstahi yule aliyevaa mavazi mazuri, na kumwambia, Keti wewe hapa mahali pazuri; na kumwambia yule maskini, Simama wewe pale, au keti miguuni pangu, 4 je! Hamkufanya hitilafu mioyoni mwenu, mkawa waamuzi wenye mawazo mabovu? 5 Ndugu zangu wapenzi, sikilizeni, Je! Mungu hakuwachagua maskini wa dunia wawe matajiri wa imani na warithi wa ufalme aliowaahidia wampendao? 6 Bali ninyi mmemvunjia heshima maskini. Je! Matajiri hawawaonei ninyi na kuwavuta mbele ya viti vya hukumu? 7 Hawalitukani jina lile zuri mliloitwa? 8 Lakini mkiitimiza ile sheria ya kifalme kama ilivyoandikwa, Mpende jirani yako kama nafsi yako, mwatenda vema. 9 Bali mkiwapendelea watu, mwafanya dhambi na kuhukumiwa na sheria kuwa wakosaji. 10 Maana mtu awaye yote atakayeishika sheria yote, ila akajikwaa katika neno moja, amekosa juu ya yote. 11 Kwa maana yeye aliyesema, Usizini, pia alisema, Usiue. Basi ijapokuwa hukuzini, lakini umeua, umekuwa mvunja sheria. 12 Semeni ninyi, na kutenda kama watu watakaohukumiwa kwa sheria ya uhuru. 13 Maana hukumu haina huruma kwake yeye asiyeona huruma. Huruma hujitukuza juu ya hukumu. 14 Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? Je! Ile imani yaweza kumwokoa? 15 Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, 16 na mtu wa kwenu akawaambia, Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini? 17 Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake. 18 Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu. 19 Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja; watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka. 20 Lakini wataka kujua, wewe mwanadamu usiye kitu, kwamba imani pasipo matendo haizai? 21 Je! Baba yetu Ibrahimu hakuhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo, hapo alipomtoa Isaka mwanawe juu ya madhabahu? 22 Waona kwamba imani ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na ya kwamba imani ile ilikamilishwa kwa njia ya matendo yale. 23 Maandiko yale yakatimizwa yaliyonena, Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa Mungu. 24 Mwaona kwamba mwanadamu huhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo yake; si kwa imani peke yake. 25 Vivyo hivyo na Rahabu, yule kahaba naye, je! Hakuhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo, hapo alipowakaribisha wajumbe, akawatoa nje kwa njia nyingine? 26 Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.

Yakobo 3

1 Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. 2 Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu. 3 Angalieni, twatia lijamu katika vinywa vya farasi, ili wamtii, hivi twageuza mwili wao wote. 4 Tena angalieni merikebu; ingawa ni kubwa kama nini, na kuchukuliwa na pepo kali, zageuzwa na usukani mdogo sana, ko kote anakoazimia kwenda nahodha. 5 Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana. 6 Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum. 7 Maana kila aina ya wanyama, na ya ndege, na ya vitambaavyo, na ya vitu vilivyomo baharini, vinafugika, navyo vimekwisha kufugwa na wanadamu. 8 Bali ulimi hakuna awezaye kuufuga; ni uovu usiotulia, umejaa sumu iletayo mauti. 9 Kwa huo twamhimidi Mungu Baba yetu, na kwa huo twawalaani wanadamu waliofanywa kwa mfano wa Mungu. 10 Katika kinywa kile kile hutoka baraka na laana. Ndugu zangu, haifai mambo hayo kuwa hivyo. 11 Je! Chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu? 12 Ndugu zangu, Je! Mtini waweza kuzaa zeituni, au mzabibu kuzaa tini? Kadhalika chemchemi haiwezi kutoa maji ya chumvi na maji matamu. 13 N'nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima. 14 Lakini, mkiwa na wivu wenye uchungu na ugomvi mioyoni mwenu, msijisifu, wala msiseme uongo juu ya kweli. 15 Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. 16 Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya. 17 Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki. 18 Na tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao amani.

Yakobo 4

1 Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu? 2 Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi! 3 Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu. 4 Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu. 5 Au mwadhani ya kwamba maandiko yasema bure? Huyo Roho akaaye ndani yetu hututamani kiasi cha kuona wivu? 6 Lakini hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu. 7 Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. 8 Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili. 9 Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu. 10 Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza. 11 Ndugu, msisingiziane; amsingiziaye ndugu yake, au kumhukumu ndugu yake, huisingizia sheria na kuihukumu sheria. Lakini ukiihukumu sheria, huwi mtenda sheria, bali umekuwa hakimu. 12 Mtoa sheria na mwenye kuhukumu ni mmoja tu, ndiye awezaye kuokoa na kuangamiza. U nani wewe umhukumuye mtu mwingine? 13 Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; 14 walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. 15 Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi. 16 Lakini sasa mwajisifu katika majivuno yenu; kujisifu kote kwa namna hii ni kubaya. 17 Basi yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi.

Yakobo 5

1 Haya basi, enyi matajiri! Lieni, mkapige yowe kwa sababu ya mashaka yenu yanayowajia. 2 Mali zenu zimeoza, na mavazi yenu yameliwa na nondo. 3 Dhahabu yenu na fedha yenu zimeingia kutu, na kutu yake itawashuhudia, nayo itakula miili yenu kama moto. Mmejiwekea akiba katika siku za mwisho. 4 Angalieni, ujira wa wakulima waliovuna mashamba yenu, ninyi mliouzuia kwa hila, unapiga kelele, na vilio vyao waliovuna vimeingia masikioni mwa Bwana wa majeshi. 5 Mmefanya anasa katika dunia, na kujifurahisha kwa tamaa; mmejilisha mioyo yenu kama siku ya machinjo. 6 Mmehukumu mwenye haki mkamwua; wala hashindani nanyi. 7 Kwa hiyo ndugu, vumilieni, hata kuja kwake Bwana. Tazama, mkulima hungoja mazao ya nchi yaliyo ya thamani, huvumilia kwa ajili yake hata yatakapopata mvua ya kwanza na ya mwisho. 8 Nanyi vumilieni, mthibitishe mioyo yenu, kwa maana kuja kwake Bwana kunakaribia. 9 Ndugu, msinung'unikiane, msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango. 10 Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu. 11 Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma. 12 Lakini zaidi ya yote, ndugu zangu, msiape, wala kwa mbingu wala kwa nchi; wala kwa kiapo kinginecho chote; bali ndiyo yenu na iwe ndiyo, na siyo yenu iwe siyo, msije mkaangukia hukumu. 13 Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? Na aombe. Ana moyo wa kuchangamka? Na aimbe zaburi. 14 Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. 15 Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa. 16 Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii. 17 Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinyeshe, na mvua haikunyesha juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita. 18 Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake. 19 Ndugu zangu, ikiwa mtu wa kwenu amepotelea mbali na kweli, na mtu mwingine akamrejeza; 20 jueni ya kuwa yeye amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu, ataokoa roho na mauti, na kufunika wingi wa dhambi.

1 Petro 1

1 Petro, mtume wa Yesu Kristo, kwa wateule wa Utawanyiko, wakaao hali ya ugeni katika Ponto, na Galatia, na Kapadokia, na Asia, na Bithinia; 2 kama vile Mungu Baba alivyotangulia kuwajua katika kutakaswa na Roho, hata mkapata kutii na kununyiziwa damu ya Yesu Kristo. Neema na amani na ziongezwe kwenu. 3 Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; 4 tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu. 5 Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu kwa njia ya imani hata mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho. 6 Mnafurahi sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali; 7 ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo. 8 Naye mwampenda, ijapokuwa hamkumwona; ambaye ijapokuwa hamwoni sasa, mnamwamini; na kufurahi sana, kwa furaha isiyoneneka, yenye utukufu, 9 katika kuupokea mwisho wa imani yenu, yaani, wokovu wa roho zenu. 10 Katika habari ya wokovu huo manabii walitafuta-tafuta na kuchunguza-chunguza, ambao walitabiri habari za neema itakayowafikia ninyi. 11 Wakatafuta ni wakati upi, na wakati wa namna gani ulioonywa na Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao, ambaye alitangulia kuyashuhudia mateso yatakayompata Kristo, na utukufu utakaokuwako baada ya hayo. 12 Wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni. Mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia. 13 Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo. 14 Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; 15 bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; 16 kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu. 17 Na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni. 18 Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; 19 bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo. 20 Naye amejulikana kweli tangu zamani, kabla haijawekwa misingi ya dunia; lakini alifunuliwa mwisho wa zamani kwa ajili yenu; 21 ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu. 22 Mkiisha kujitakasa roho zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi jitahidini kupendana kwa moyo. 23 Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele. 24 Maana, Mwili wote ni kama majani, Na fahari yake yote ni kama ua la majani. Majani hukauka na ua lake huanguka; 25 Bali Neno la Bwana hudumu hata milele. Na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu.

1 Petro 2

1 Basi, wekeni mbali uovu wote na hila yote, na unafiki na husuda na masingizio yote. 2 Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu; 3 ikiwa mmeonja ya kwamba Bwana ni mwenye fadhili. 4 Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. 5 Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. 6 Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika. 7 Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni. 8 Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo. 9 Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; 10 ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema. 11 Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho. 12 Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa. 13 Tiini kila kiamriwacho na watu, kwa ajili ya Bwana; ikiwa ni mfalme, kama mwenye cheo kikubwa; 14 ikiwa ni wakubwa, kama wanaotumwa naye ili kuwalipiza kisasi watenda mabaya na kuwasifu watenda mema. 15 Kwa sababu ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba kwa kutenda mema mzibe vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu; 16 kama walio huru, ila wasioutumia uhuru huo kwa kusitiri ubaya, bali kama watumwa wa Mungu. 17 Waheshimuni watu wote. Wapendeni ndugu. Mcheni Mungu. Mpeni heshima mfalme. 18 Enyi watumishi, watiini bwana zenu kwa hofu nyingi, sio wao walio wema na wenye upole tu, bali nao walio wakali. 19 Maana huu ndio wema hasa, mtu akivumilia huzuni kwa kumkumbuka Mungu, pale ateswapo isivyo haki. 20 Kwa maana ni sifa gani kustahimili, mtendapo dhambi na kupigwa makofi? Lakini kustahimili, mtendapo mema na kupata mateso, huu ndio wema hasa mbele za Mungu. 21 Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake. 22 Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. 23 Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. 24 Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa. 25 Kwa maana mlikuwa mnapotea kama kondoo; lakini sasa mmemrudia Mchungaji na Mwangalizi wa roho zenu.

1 Petro 3

1 Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno; 2 wakiutazama mwenendo wenu safi, na wa hofu. 3 Kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu, na kuvalia mavazi; 4 bali kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani, roho ya upole na utulivu, iliyo ya thamani kuu mbele za Mungu. 5 Maana hivyo ndivyo walivyojipamba wanawake watakatifu wa zamani, waliomtumaini Mungu, na kuwatii waume zao. 6 Kama vile Sara alivyomtii Ibrahimu, akamwita Bwana; nanyi ni watoto wake, mfanyapo mema, wala hamkutishwa kwa hofu yo yote. 7 Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe. 8 Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu; 9 watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka. 10 Kwa maana, Atakaye kupenda maisha, Na kuona siku njema, Auzuie ulimi wake usinene mabaya, Na midomo yake isiseme hila. 11 Na aache mabaya, atende mema; Atafute amani, aifuate sana. 12 Kwa kuwa macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake husikiliza maombi yao; Bali uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya. 13 Naye ni nani atakayewadhuru, mkiwa wenye juhudi katika mema? 14 Lakini mjapoteswa kwa sababu ya haki mna heri. Msiogope kutisha kwao, wala msifadhaike; bali mtakaseni Kristo Bwana mioyoni mwenu. 15 Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu. 16 Nanyi mwe na dhamiri njema, ili katika neno lile mnalosingiziwa, watahayarishwe wale wautukanao mwenendo wenu mwema katika Kristo. 17 Maana ni afadhali kuteswa kwa kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa kutenda mabaya. 18 Kwa maana Kristo naye aliteswa mara moja kwa ajili ya dhambi, mwenye haki kwa ajili yao wasio haki, ili atulete kwa Mungu; mwili wake akauawa, bali roho yake akahuishwa, 19 ambayo kwa hiyo aliwaendea roho waliokaa kifungoni, akawahubiri; 20 watu wasiotii hapo zamani, uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Nuhu, safina ilipokuwa ikitengenezwa; ambamo ndani yake wachache, yaani, watu wanane, waliokoka kwa maji. 21 Mfano wa mambo hayo ni ubatizo, unaowaokoa ninyi pia siku hizi; (siyo kuwekea mbali uchafu wa mwili, bali jibu la dhamiri safi mbele za Mungu), kwa kufufuka kwake Yesu Kristo. 22 Naye yupo mkono wa kuume wa Mungu, amekwenda zake mbinguni, malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.

1 Petro 4

1 Basi kwa kuwa Kristo aliteswa katika mwili wake, ninyi nanyi jivikeni silaha ya nia ile ile; kwa maana yeye aliyeteswa katika mwili ameachana na dhambi. 2 Tangu sasa msiendelee kuishi katika tamaa za wanadamu, bali katika mapenzi ya Mungu, wakati wenu uliobaki wa kukaa hapa duniani. 3 Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali; 4 mambo ambayo wao huona kuwa ni ajabu ya ninyi kutokwenda mbio pamoja nao katika ufisadi ule ule usio na kiasi, wakiwatukana. 5 Nao watatoa hesabu kwake yeye aliye tayari kuwahukumu walio hai na waliokufa. 6 Maana kwa ajili hiyo hata hao waliokufa walihubiriwa Injili, ili kwamba wahukumiwe katika mwili kama wahukumiwavyo wanadamu; bali wawe hai katika roho kama Mungu alivyo hai. 7 Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala. 8 Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. 9 Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung'unika; 10 kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu. 11 Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina. 12 Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. 13 Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe. 14 Mkilaumiwa kwa ajili ya jina la Kristo ni heri yenu; kwa kuwa Roho wa utukufu na wa Mungu anawakalia. 15 Maana mtu wa kwenu asiteswe kama mwuaji, au mwivi, au mtenda mabaya, au kama mtu ajishughulishaye na mambo ya watu wengine. 16 Lakini ikiwa kwa sababu ni Mkristo asione haya, bali amtukuze Mungu katika jina hilo. 17 Kwa maana wakati umefika wa hukumu kuanza katika nyumba ya Mungu; na ikianza kwetu sisi, mwisho wao wasioitii injili ya Mungu utakuwaje? 18 Na mwenye haki akiokoka kwa shida, yule asiyemcha Mungu na mwenye dhambi ataonekana wapi? 19 Basi wao wateswao kwa mapenzi ya Mungu na wamwekee amana roho zao, katika kutenda mema, kama kwa Muumba mwaminifu.

1 Petro 5

1 Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; 2 lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. 3 Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi. 4 Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka. 5 Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. 6 Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; 7 huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu. 8 Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. 9 Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani. 10 Na Mungu wa neema yote, aliyewaita kuingia katika utukufu wake wa milele katika Kristo, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu. 11 Uweza una yeye hata milele na milele. Amina. 12 Kwa mkono wa Silwano, ndugu mwaminifu kama nionavyo, nimewaandikia kwa maneno machache, kuonya na kushuhudia ya kuwa hii ndiyo neema ya kweli ya Mungu. Simameni imara katika hiyo. 13 Mwenzenu mteule hapa Babeli awasalimu, na Marko mwanangu. 14 Salimianeni kwa busu la upendo. Amani na iwe kwenu nyote, mlio katika Kristo. Amina.

2 Petro 1

1 Simoni Petro, mtumwa na mtume wa Yesu Kristo, kwa wale waliopata imani moja na sisi, yenye thamani, katika hali ya Mungu wetu, na Mwokozi Yesu Kristo. 2 Neema na iwe kwenu na amani iongezwe katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu. 3 Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. 4 Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa. 5 Naam, na kwa sababu iyo hiyo mkijitahidi sana kwa upande wenu, katika imani yenu tieni na wema, na katika wema wenu maarifa, 6 na katika maarifa yenu kiasi, na katika kiasi chenu saburi, na katika saburi yenu utauwa, 7 na katika utauwa wenu upendano wa ndugu, na katika upendano wa ndugu, upendo. 8 Maana mambo hayo yakiwa kwenu na kujaa tele, yawafanya ninyi kuwa si wavivu wala si watu wasio na matunda, kwa kumjua Bwana wetu Yesu Kristo. 9 Maana yeye asiyekuwa na hayo ni kipofu, hawezi kuona vitu vilivyo mbali, amesahau kule kutakaswa dhambi zake za zamani. 10 Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe. 11 Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo. 12 Kwa hiyo nitakuwa tayari kuwakumbusha hayo siku zote, ijapokuwa mnayajua na kuthibitishwa katika kweli mliyo nayo. 13 Nami naona ni haki, maadamu nipo mimi katika maskani hii, kuwaamsha kwa kuwakumbusha. 14 Nikijua kwamba kule kuwekea mbali maskani yangu kwaja upesi, kama Bwana wetu Yesu Kristo alivyonionyesha. 15 Walakini nitajitahidi, kwamba kila wakati baada ya kufariki kwangu mpate kuyakumbuka mambo hayo. 16 Maana hatukufuata hadithi zilizotungwa kwa werevu, tulipowajulisha ninyi nguvu zake Bwana wetu Yesu Kristo na kuja kwake; bali tulikuwa tumeuona wenyewe ukuu wake. 17 Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye. 18 Na sauti hiyo sisi tuliisikia ikitoka mbinguni tulipokuwa pamoja naye katika mlima ule mtakatifu. 19 Nasi tuna lile neno la unabii lililo imara zaidi, ambalo, mkiliangalia, kama taa ing'aayo mahali penye giza, mwafanya vyema, mpaka kutakapopambazuka, na nyota ya asubuhi kuzuka mioyoni mwenu. 20 Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. 21 Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu.

2 Petro 2

1 Lakini kuliondokea manabii wa uongo katika wale watu, kama vile kwenu kutakavyokuwako waalimu wa uongo, watakaoingiza kwa werevu uzushi wa kupoteza, wakimkana hata Bwana aliyewanunua, wakijiletea uharibifu usiokawia. 2 Na wengi watafuata ufisadi wao; na kwa hao njia ya kweli itatukanwa. 3 Na katika kutamani watajipatia faida kwenu kwa maneno yaliyotungwa; ambao hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii. 4 Kwa maana ikiwa Mungu hakuwaachilia malaika waliokosa, bali aliwatupa shimoni, akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu; 5 wala hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu, mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta Gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu; 6 tena akaihukumu miji ya Sodoma na Gomora, akiipindua na kuifanya majivu, akaifanya iwe ishara kwa watu watakaokuwa hawamchi Mungu baada ya haya; 7 akamwokoa Lutu, yule mwenye haki aliyehuzunishwa sana na mwenendo wa ufisadi wa hao wahalifu; 8 maana mtu huyu mwenye haki akikaa kati yao, kwa kuona na kusikia, alijitesa roho yake yenye haki, siku baada ya siku, kwa matendo yao yasiyo na sheria; 9 basi, Bwana ajua kuwaokoa watauwa na majaribu, na kuwaweka wasio haki katika hali ya adhabu hata siku ya hukumu; 10 na hasa wale waufuatao mwili katika tamaa ya mambo machafu. na kudharau mamlaka. 11 Wenye ushupavu, wenye kujikinai, hawatetemeki wakiyatukana matukufu; ijapokuwa malaika ambao ni wakuu zaidi kwa uwezo na nguvu, hawaleti mashitaka mabaya juu yao mbele za Bwana. 12 Lakini hao kama wanyama wasio na akili, ambao walizaliwa kama wanyama tu wa kukamatwa na kupotezwa, wakikufuru katika mambo wasiyoyajua, wataangamizwa katika maangamizo yao; 13 Wakipatikana na madhara, ambayo ni ujira wa udhalimu wao, wakidhania kuwa ulevi wakati wa mchana ni anasa; wamekuwa ni mawaa na aibu wakifuata anasa zisizo kiasi katika karamu zao za upendo, wafanyapo karamu pamoja nanyi; 14 wenye macho yajaayo uzinzi, watu wasiokoma kutenda dhambi, wenye kuhadaa roho zisizo imara, wenye mioyo iliyozoezwa kutamani, wana wa laana; 15 wakiiacha njia iliyonyoka, wakapotea, wakiifuata njia ya Balaamu, mwana wa Beori, aliyependa ujira wa udhalimu; 16 lakini alikaripiwa kwa uhalifu wake mwenyewe; punda, asiyeweza kusema, akinena kwa sauti ya kibinadamu, aliuzuia wazimu wa nabii yule. 17 Hawa ni visima visivyo na maji, na mawingu yachukuliwayo na tufani, ambao weusi wa giza ni akiba waliyowekewa. 18 Maana wakinena maneno makuu mno ya kiburi, kwa tamaa za mwili na kwa ufisadi huwahadaa watu walioanza kuwakimbia wale wanaoenenda katika udanganyifu; 19 wakiwaahidia uhuru, nao wenyewe ni watumwa wa uharibifu, maana mtu akishindwa na mtu huwa mtumwa wa mtu yule. 20 Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza. 21 Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki, kuliko kuijua, kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa. 22 Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni.

2 Petro 3

1 Wapenzi, waraka huu ndio wa pili niwaandikiao ninyi; katika zote mbili naziamsha nia zenu safi kwa kuwakumbusha, 2 mpate kuyakumbuka yale maneno yaliyonenwa zamani na manabii watakatifu, na ile amri ya Bwana na Mwokozi iliyoletwa na mitume wenu. 3 Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, 4 na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa. 5 Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu; 6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia. 7 Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu. 8 Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja. 9 Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba. 10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea. 11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, 12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? 13 Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake. 14 Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake. 15 Nanyi uhesabuni uvumilivu wa Bwana wetu kuwa ni wokovu, kama vile na ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa; 16 vile vile kama katika nyaraka zake zote pia, akitoa humo habari za mambo hayo; katika nyaraka hizo yamo mambo ambayo ni vigumu kuelewa nayo; na mambo hayo watu wasio na elimu, wasio imara, huyapotoa, kama vile wayapotoavyo na maandiko mengine, kwa uvunjifu wao wenyewe. 17 Basi, wapenzi mkitangulia kujua hayo, jilindeni nafsi zenu, msije mkachukuliwa na kosa la hao wahalifu mkaanguka na kuuacha uthibitifu wenu. 18 Lakini, kueni katika neema, na katika kumjua Bwana wetu na Mwokozi Yesu Kristo. Utukufu una yeye sasa na hata milele.

1 Yohana 1

1 Lile lililokuwako tangu mwanzo, tulilolisikia, tuliloliona kwa macho yetu, tulilolitazama, na mikono yetu ikalipapasa, kwa habari ya Neno la uzima; 2 (na uzima huo ulidhihirika, nasi tumeona, tena twashuhudia, na kuwahubiri ninyi ule uzima wa milele, uliokuwa kwa Baba, ukadhihirika kwetu); 3 hilo tuliloliona na kulisikia, twawahubiri na ninyi; ili nanyi pia mpate kushirikiana nasi: na ushirika wetu ni pamoja na Baba, na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo. 4 Na haya twayaandika, ili furaha yetu itimizwe. 5 Na hii ndiyo habari tuliyoisikia kwake, na kuihubiri kwenu, ya kwamba Mungu ni nuru, wala giza lo lote hamna ndani yake. 6 Tukisema ya kwamba twashirikiana naye, tena tukienenda gizani, twasema uongo, wala hatuifanyi iliyo kweli; 7 bali tukienenda nuruni, kama yeye alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote. 8 Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu. 9 Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote. 10 Tukisema kwamba hatukutenda dhambi, twamfanya Yeye kuwa mwongo wala neno lake halimo mwetu.

1 Yohana 2

1 Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, 2 naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote. 3 Na katika hili twajua ya kuwa tumemjua yeye, ikiwa tunashika amri zake. 4 Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake. 5 Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake. 6 Yeye asemaye ya kuwa anakaa ndani yake, imempasa kuenenda mwenyewe vile vile kama yeye alivyoenenda. 7 Wapenzi, siwaandikii amri mpya, ila amri ya zamani mliyokuwa nayo tangu mwanzo. Na hiyo amri ya zamani ni neno lile mlilolisikia. 8 Tena nawaandikia amri mpya, neno lililo kweli ndani yake na ndani yenu; kwa kuwa giza linapita na ile nuru ya kweli imekwisha kung'aa. 9 Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. 10 Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. 11 Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho. 12 Nawaandikia ninyi, watoto wadogo, kwa sababu mmesamehewa dhambi zenu, kwa ajili ya jina lake. 13 Nawaandikia ninyi, akina baba, kwa sababu mmemjua yeye aliye tangu mwanzo. Nawaandikia ninyi, vijana, kwa sababu mmemshinda yule mwovu. Nimewaandikia ninyi, watoto, kwa sababu mmemjua Baba. 14 Nimewaandikia ninyi, akina baba, kwa sababu mmemjua yeye aliye tangu mwanzo. Nimewaandikia ninyi, vijana, kwa sababu mna nguvu, na neno la Mungu linakaa ndani yenu, nanyi mmemshinda yule mwovu. 15 Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. 16 Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. 17 Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele. 18 Watoto, ni wakati wa mwisho; na kama vile mlivyosikia kwamba mpinga Kristo yuaja, hata sasa wapinga Kristo wengi wamekwisha kuwapo. Kwa sababu hiyo twajua ya kuwa ni wakati wa mwisho. 19 Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi. Lakini walitoka ili wafunuliwe kwamba si wote walio wa kwetu. 20 Nanyi mmepakwa mafuta na Yeye aliye Mtakatifu nanyi mnajua nyote. 21 Sikuwaandikia ninyi kwa sababu hamwijui iliyo kweli, bali kwa sababu mwaijua, tena kwamba hapana uongo wo wote utokao katika hiyo kweli. 22 Ni nani aliye mwongo ila yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo? Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana. 23 Kila amkanaye Mwana, hanaye Baba; amkiriye Mwana anaye Baba pia. 24 Ninyi basi, hilo mlilolisikia tangu mwanzo na likae ndani yenu. Ikiwa hilo mlilolisikia tangu mwanzo linakaa ndani yenu, ninyi nanyi mtakaa ndani ya Mwana, na ndani ya Baba. 25 Na hii ndiyo ahadi aliyotuahidia, yaani, uzima wa milele. 26 Nimewaandikia haya katika habari za watu wale wanaotaka kuwapoteza. 27 Nanyi, mafuta yale mliyoyapata kwake yanakaa ndani yenu, wala hamna haja ya mtu kuwafundisha; lakini kama mafuta yake yanavyowafundisha habari za mambo yote, tena ni kweli wala si uongo, na kama yalivyowafundisha, kaeni ndani yake. 28 Na sasa, watoto wadogo, kaeni ndani yake, ili kusudi, atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala msiaibike mbele zake katika kuja kwake. 29 Kama mkijua ya kuwa yeye ni mwenye haki, jueni ya kuwa kila atendaye haki amezaliwa na yeye.

1 Yohana 3

1 Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye. 2 Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. 3 Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu. 4 Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi. 5 Nanyi mnajua ya kuwa yeye alidhihirishwa, ili aziondoe dhambi; na dhambi haimo ndani yake. 6 Kila akaaye ndani yake hatendi dhambi; kila atendaye dhambi hakumwona yeye, wala hakumtambua. 7 Watoto wadogo, mtu na asiwadanganye; atendaye haki yuna haki, kama yeye alivyo na haki; 8 atendaye dhambi ni wa Ibilisi; kwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu mwanzo. Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi. 9 Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao wake wakaa ndani yake; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu. 10 Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake. 11 Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi; 12 si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake. Naye alimwua kwa sababu gani? Kwa sababu matendo yake yalikuwa mabaya, na ya ndugu yake yalikuwa ya haki. 13 Ndugu zangu, msistaajabu, ulimwengu ukiwachukia. 14 Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti. 15 Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji: nanyi mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake. 16 Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu. 17 Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo? 18 Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli. 19 Katika hili tutafahamu ya kwamba tu wa kweli, nasi tutaituliza mioyo yetu mbele zake, 20 ikiwa mioyo yetu inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote. 21 Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; 22 na lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake. 23 Na hii ndiyo amri yake, kwamba tuliamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana sisi kwa sisi, kama alivyotupa amri. 24 Naye azishikaye amri zake hukaa ndani yake yeye naye ndani yake. Na katika hili tunajua ya kuwa anakaa ndani yetu, kwa huyo Roho aliyetupa.

1 Yohana 4

1 Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani. 2 Katika hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili yatokana na Mungu. 3 Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu. Na hii ndiyo roho ya mpinga Kristo ambayo mmesikia kwamba yaja; na sasa imekwisha kuwako duniani. 4 Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia. 5 Hao ni wa dunia; kwa hiyo wanena ya dunia na dunia huwasikia 6 Sisi twatokana na Mungu. Yeye amjuaye Mungu atusikia; yeye asiyetokana na Mungu hatusikii. Katika hili twamjua Roho wa kweli, na roho ya upotevu. 7 Wapenzi, na mpendane; kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, na kila apendaye amezaliwa na Mungu, naye anamjua Mungu. 8 Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. 9 Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. 10 Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. 11 Wapenzi ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana. 12 Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote. Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu. 13 Katika hili tunafahamu ya kuwa tunakaa ndani yake, naye ndani yetu, kwa kuwa ametushirikisha Roho wake. 14 Na sisi tumeona na kushuhudia ya kuwa Baba amemtuma Mwana kuwa Mwokozi wa ulimwengu. 15 Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. 16 Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake. 17 Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu. 18 Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu; na mwenye hofu hakukamilishwa katika pendo. 19 Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza. 20 Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. 21 Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.

1 Yohana 5

1 Kila mtu aaminiye kwamba Yesu ni Kristo amezaliwa na Mungu. Na kila mtu ampendaye mwenye kuzaa, ampenda hata yeye aliyezaliwa na yeye. 2 Katika hili twajua kwamba twawapenda watoto wa Mungu, tumpendapo Mungu, na kuzishika amri zake. 3 Kwa maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito. 4 Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu. 5 Mwenye kuushinda ulimwengu ni nani, isipokuwa ni yeye aaminiye ya kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu? 6 Huyu ndiye aliyekuja kwa maji na damu, Yesu Kristo; si katika maji tu, bali katika maji na katika damu. 7 Naye Roho ndiye ashuhudiaye, kwa sababu Roho ndiye kweli. 8 Kwa maana wako watatu washuhudiao mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja. 9 Kisha wako watatu washuhudiao duniani, Roho, na maji, na damu; na watatu hawa hupatana kwa habari moja. Tukiupokea ushuhuda wa wanadamu, ushuhuda wa Mungu ni mkuu zaidi; kwa maana ushuhuda wa Mungu ndio huu, kwamba amemshuhudia Mwanawe. 10 Yeye amwaminiye Mwana wa Mungu anao huo ushuhuda ndani yake. Asiyemwamini Mungu amemfanya kuwa mwongo, kwa kuwa hakuuamini huo ushuhuda ambao Mungu amemshuhudia Mwanawe. 11 Na huu ndio ushuhuda, ya kwamba Mungu alitupa uzima wa milele; na uzima huu umo katika Mwanawe. 12 Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima. 13 Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu. 14 Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia. 15 Na kama tukijua kwamba atusikia, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba. 16 Mtu akimwona ndugu yake anatenda dhambi isiyo ya mauti, ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya mauti. Iko dhambi iliyo ya mauti. Sisemi ya kwamba ataomba kwa ajili ya hiyo. 17 Kila lisilo la haki ni dhambi, na dhambi iko isiyo ya mauti. 18 Twajua ya kuwa kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu hujilinda, wala yule mwovu hamgusi. 19 Twajua ya kuwa sisi tu wa Mungu; na dunia yote pia hukaa katika yule mwovu. 20 Nasi twajua kwamba Mwana wa Mungu amekwisha kuja, naye ametupa akili kwamba tumjue yeye aliye wa kweli, nasi tumo ndani yake yeye aliye wa kweli, yaani, ndani ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na uzima wa milele. 21 Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu.

2 Yohana 1

1 Mzee, kwa mama mteule na watoto wake niwapendao katika kweli; wala si mimi peke yangu, bali na wote waijuao ile kweli; 2 kwa ajili ya hiyo kweli ikaayo ndani yetu, nayo itakuwa pamoja nasi hata milele. 3 Neema, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Yesu Kristo Mwana wa Baba, zitakuwa pamoja nasi katika kweli na upendo. 4 Nalifurahi mno kwa kuwa nimewaona baadhi ya watoto wako wanaenenda katika kweli, kama vile tulivyopokea amri kwa Baba. 5 Na sasa mama, nakuomba, si kwamba nakuandikia amri mpya, bali ile tuliyokuwa nayo tangu mwanzo, kwamba tupendane. 6 Na huu ndio upendo: tuenende kwa kuzifuata amri zake. Hii ndiyo ile amri, kama mlivyosikia tangu mwanzo kwamba mwenende katika hiyo. 7 Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea duniani, wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu na mpinga Kristo. 8 Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze mliyoyatenda, bali mpokee thawabu timilifu. 9 Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia. 10 Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. 11 Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu. 12 Kwa kuwa ninayo mambo mengi, sitaki kuyaandika kwa karatasi na wino; lakini nataraji kuja kwenu, na kusema nanyi uso kwa uso, ili furaha yetu iwe imetimizwa. 13 Watoto wa ndugu yako aliye mteule, wakusalimu.

3 Yohana 1

1 Mzee, kwa Gayo mpenzi, nimpendaye katika kweli. 2 Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo. 3 Maana nalifurahi mno walipokuja ndugu na kuishuhudia kweli yako, kama uendavyo katika kweli. 4 Sina furaha iliyo kuu kuliko hii, kusikia ya kwamba watoto wangu wanakwenda katika kweli. 5 Mpenzi, kazi ile ni ya uaminifu uwatendeayo hao ndugu na hao wageni nao, 6 waliokushuhudia upendo wako mbele ya kanisa; utafanya vizuri ukiwasafirisha kama ipasavyo kwa Mungu. 7 Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa. 8 Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli. 9 Naliliandikia kanisa neno, lakini Diotrefe, apendaye kuwa wa kwanza kati yao, hatukubali. 10 Kwa hiyo, nikija, nitayakumbuka matendo yake atendayo, atoavyo upuzi juu yetu kwa maneno maovu; wala hatoshwi na hayo, ila yeye mwenyewe hawakaribishi hao ndugu, na wale watakao kuwakaribisha, huwazuia, na kuwatoa katika kanisa. 11 Mpenzi, usiuige ubaya, bali uige wema. Yeye atendaye mema ni wa Mungu, bali yeye atendaye mabaya hakumwona Mungu. 12 Demetrio ameshuhudiwa na watu wote, tena na ile kweli yenyewe. Nasi pia twashuhudia, nawe wajua ya kwamba ushuhuda wetu ni kweli. 13 Nalikuwa na mambo mengi ya kukuandikia, lakini sipendi kukuandikia kwa wino na kalamu. 14 Lakini nataraji kukuona karibu, nasi tutasema uso kwa uso. 15 Amani kwako. Rafiki zetu wakusalimu. Wasalimu hao rafiki zetu, kila mtu kwa jina lake.

Yuda 1

1 Yuda, mtumwa wa Yesu Kristo, ndugu yake Yakobo, kwa hao walioitwa, waliopendwa katika Mungu Baba, na kuhifadhiwa kwa ajili ya Yesu Kristo. 2 Mwongezewe rehema na amani na upendano. 3 Wapenzi, nilipokuwa nikifanya bidii sana kuwaandikia habari ya wokovu ambao ni wetu sisi sote, naliona imenilazimu kuwaandikia, ili niwaonye kwamba mwishindanie imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu. 4 Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo. 5 Tena napenda kuwakumbusha, ijapokuwa mmekwisha kujua haya yote, ya kwamba Bwana, akiisha kuwaokoa watu katika nchi ya Misri, aliwaangamiza baadaye wale wasioamini. 6 Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu. 7 Kama vile Sodoma na Gomora na miji iliyokuwa kando-kando, waliofuata uasherati kwa jinsi moja na hawa, wakaenda kufuata mambo ya mwili yasiyo ya asili, imewekwa kuwa dalili, wakiadhibiwa katika moto wa milele. 8 Kadhalika na hawa, katika kuota kwao, huutia mwili uchafu, hukataa kutawaliwa, na kuyatukana matukufu. 9 Lakini Mikaeli, malaika mkuu, aliposhindana na Ibilisi, na kuhojiana naye kwa ajili ya mwili wa Musa, hakuthubutu kumshitaki kwa kumlaumu, bali alisema, Bwana na akukemee. 10 Lakini watu hawa huyatukana mambo wasiyoyajua, na mambo wayatambuayo kwa asili wajiharibu kwayo kama wanyama wasio na akili. 11 Ole wao! Kwa sababu walikwenda katika njia ya Kaini, na kulifuata kosa la Balaamu pasipo kujizuia, kwa ajili ya ujira, nao wameangamia katika maasi ya Kora. 12 Watu hawa ni miamba yenye hatari katika karamu zenu za upendo walapo karamu pamoja nanyi, wakijilisha pasipo hofu; ni mawingu yasiyo na maji, yachukuliwayo na upepo; ni miti iliyopukutika, isiyo na matunda, iliyokufa mara mbili, na kung'olewa kabisa; 13 ni mawimbi ya bahari yasiyozuilika, yakitoa aibu yao wenyewe kama povu; ni nyota zipoteazo, ambao weusi wa giza ndio akiba yao waliowekewa milele. 14 Na Henoko, mtu wa saba baada ya Adamu, alitoa maneno ya unabii juu ya hao, akisema, Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu, 15 ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake. 16 Watu hawa ni wenye kunung'unika, wenye kulalamika, waendao kwa tamaa zao, na vinywa vyao vyanena maneno makuu mno ya kiburi, wakipendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida. 17 Bali ninyi, wapenzi, yakumbukeni maneno yaliyonenwa zamani na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo, 18 ya kwamba waliwaambia ya kuwa, Wakati wa mwisho watakuwako watu wenye kudhihaki, wakizifuata tamaa zao wenyewe za upotevu. 19 Watu hao ndio waletao matengano, watu wa dunia hii tu, wasio na Roho. 20 Bali ninyi, wapenzi, mkijijenga juu ya imani yenu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu, 21 jilindeni katika upendo wa Mungu, huku mkingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo, hata mpate uzima wa milele. 22 Wahurumieni wengine walio na shaka, 23 na wengine waokoeni kwa kuwanyakua katika moto; na wengine wahurumieni kwa hofu, mkilichukia hata vazi lililotiwa uchafu na mwili. 24 Yeye awezaye kuwalinda ninyi msijikwae, na kuwasimamisha mbele ya utukufu wake bila mawaa katika furaha kuu; 25 Yeye aliye Mungu pekee, Mwokozi wetu kwa Yesu Kristo Bwana wetu; utukufu una yeye, na ukuu, na uwezo, na nguvu, tangu milele, na sasa, na hata milele. Amina.

Ufunuo 1

1 Ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu awaonyeshe watumwa wake mambo ambayo kwamba hayana budi kuwako upesi; naye akatuma kwa mkono wa malaika akamwonyesha mtumwa wake Yohana; 2 aliyelishuhudia Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu Kristo, yaani, mambo yote aliyoyaona. 3 Heri asomaye na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu. 4 Yohana, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia; Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi; 5 tena zitokazo kwa Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, 6 na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele. Amina. 7 Tazama, yuaja na mawingu; na kila jicho litamwona, na hao waliomchoma; na kabila zote za dunia wataomboleza kwa ajili yake. Naam. Amina. 8 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, asema Bwana Mungu, aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja, Mwenyezi. 9 Mimi Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo, kwa ajili ya Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu. 10 Nalikuwa katika Roho, siku ya Bwana; nikasikia sauti kuu nyuma yangu, kama sauti ya baragumu, 11 ikisema, Haya uyaonayo uyaandike katika chuo, ukayapeleke kwa hayo makanisa saba: Efeso, na Smirna, na Pergamo, na Thiatira, na Sardi, na Filadelfia, na Laodikia. 12 Nikageuka niione ile sauti iliyosema nami. Na nilipogeuka, niliona vinara vya taa saba vya dhahabu; 13 na katikati ya vile vinara nikaona mtu mfano wa Mwanadamu, amevaa vazi lililofika miguuni, na kufungwa mshipi wa dhahabu matitini. 14 Kichwa chake na nywele zake zilikuwa nyeupe kama sufu nyeupe, kama theluji; na macho yake kama mwali wa moto; 15 na miguu yake kama shaba iliyosuguliwa sana, kana kwamba imesafishwa katika tanuru; na sauti yake kama sauti ya maji mengi. 16 Naye alikuwa na nyota saba katika mkono wake wa kuume; na upanga mkali, wenye makali kuwili, ukitoka katika kinywa chake; na uso wake kama jua liking'aa kwa nguvu zake. 17 Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, 18 na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu. 19 Basi, uyaandike mambo hayo uliyoyaona, nayo yaliyopo, na yale yatakayokuwa baada ya hayo. 20 Siri ya zile nyota saba ulizoziona katika mkono wangu wa kuume, na ya vile vinara saba vya dhahabu. Zile nyota saba ni malaika wa yale makanisa saba; na vile vinara saba ni makanisa saba.

Ufunuo 2

1 Kwa malaika wa kanisa lililoko Efeso andika; Haya ndiyo anenayo yeye azishikaye hizo nyota saba katika mkono wake wa kuume, yeye aendaye katikati ya vile vinara saba vya dhahabu. 2 Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo; 3 tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka. 4 Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. 5 Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu. 6 Lakini unalo neno hili, kwamba wayachukia matendo ya Wanikolai, ambayo na mimi nayachukia. 7 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye, nitampa kula matunda ya mti wa uzima, ulio katika bustani ya Mungu. 8 Na kwa malaika wa kanisa lililoko Smirna andika; Haya ndiyo aneneyo yeye aliye wa kwanza na wa mwisho, aliyekuwa amekufa, kisha akawa hai. 9 Naijua dhiki yako na umaskini wako, (lakini u tajiri) najua na matukano ya hao wasemao ya kuwa ni Wayahudi, nao sio, bali ni sinagogi la Shetani. 10 Usiogope mambo yatakayokupata; tazama, huyo Ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima. 11 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye hatapatikana na madhara ya mauti ya pili. 12 Na kwa malaika wa kanisa lililoko Pergamo andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye na huo upanga mkali, wenye makali kuwili. 13 Napajua ukaapo, ndipo penye kiti cha enzi cha Shetani; nawe walishika sana jina langu, wala hukuikana imani yangu, hata katika siku za Antipa shahidi wangu, mwaminifu wangu, aliyeuawa kati yenu, hapo akaapo Shetani. 14 Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini. 15 Vivyo hivyo wewe nawe unao watu wayashikao mafundisho ya Wanikolai vile vile. 16 Basi tubu; na usipotubu, naja kwako upesi, nami nitafanya vita juu yao kwa huo upanga wa kinywa changu. 17 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye nitampa baadhi ya ile mana iliyofichwa, nami nitampa jiwe jeupe, na juu ya jiwe hilo limeandikwa jina jipya asilolijua mtu ila yeye anayelipokea. 18 Na kwa malaika wa kanisa lililoko Thiatira andika; Haya ndiyo anenayo Mwana wa Mungu, yeye aliye na macho yake kama mwali wa moto, na miguu yake mfano wa shaba iliyosuguliwa sana. 19 Nayajua matendo yako na upendo na imani na huduma na subira yako; tena kwamba matendo yako ya mwisho yamezidi yale ya kwanza. 20 Lakini nina neno juu yako, ya kwamba wamridhia yule mwanamke Yezebeli, yeye ajiitaye nabii na kuwafundisha watumishi wangu na kuwapoteza, ili wazini na kula vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu. 21 Nami nimempa muda ili atubu, wala hataki kuutubia uzinzi wake. 22 Tazama, nitamtupa juu ya kitanda, na hao wazinio pamoja naye, wapate dhiki kubwa wasipotubia matendo yake; 23 nami nitawaua watoto wake kwa mauti. Na makanisa yote watajua ya kuwa mimi ndiye achunguzaye viuno na mioyo. Nami nitampa kila mmoja wenu kwa kadiri ya matendo yake. 24 Lakini nawaambia ninyi wengine mlioko Thiatira, wo wote wasio na mafundisho hayo, wasiozijua fumbo za Shetani, kama vile wasemavyo, Sitaweka juu yenu mzigo mwingine. 25 Ila mlicho nacho kishikeni sana, hata nitakapokuja. 26 Na yeye ashindaye, na kuyatunza matendo yangu hata mwisho, nitampa mamlaka juu ya mataifa, 27 naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, kama vyombo vya mfinyanzi vipondwavyo, kama mimi nami nilivyopokea kwa Baba yangu. 28 Nami nitampa ile nyota ya asubuhi. 29 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.

Ufunuo 3

1 Na kwa malaika wa kanisa lililoko Sardi andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye na hizo Roho saba za Mungu, na zile nyota saba. Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa hai, nawe umekufa. 2 Uwe mwenye kukesha, ukayaimarishe mambo yaliyosalia, yanayotaka kufa. Maana sikuona matendo yako kuwa yametimilika mbele za Mungu wangu. 3 Basi kumbuka jinsi ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu. Walakini usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja kwako. 4 Lakini unayo majina machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu. Nao watakwenda pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa kuwa wamestahili. 5 Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe, wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele ya malaika zake. 6 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. 7 Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye. 8 Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu. 9 Tazama, nakupa walio wa sinagogi la Shetani, wasemao kwamba ni Wayahudi, nao sio, bali wasema uongo. Tazama, nitawafanya waje kusujudu mbele ya miguu yako, na kujua ya kuwa nimekupenda. 10 Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi. 11 Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako. 12 Yeye ashindaye, nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, wala hatatoka humo tena kabisa, nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya. 13 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. 14 Na kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu. 15 Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. 16 Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu. 17 Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi. 18 Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona. 19 Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu. 20 Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami. 21 Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi. 22 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.

Ufunuo 4

1 Baada ya hayo naliona, na tazama, mlango ukafunguka mbinguni, na sauti ile ya kwanza niliyoisikia kama sauti ya baragumu ikinena nami, ikisema, Panda hata huku, nami nitakuonyesha mambo ambayo hayana budi kuwako baada ya hayo. 2 Na mara nalikuwa katika Roho; na tazama, kiti cha enzi kimewekwa mbinguni na mmoja ameketi juu ya kile kiti; 3 na yeye aliyeketi alionekana mithili ya jiwe la yaspi na akiki, na upinde wa mvua ulikizunguka kile kiti cha enzi, ukionekana mithili ya zumaridi. 4 Na viti ishirini na vinne vilikizunguka kile kiti cha enzi, na juu ya vile viti naliona wazee ishirini na wanne, wameketi, wamevikwa mavazi meupe; na juu ya vichwa vyao walikuwa na taji za dhahabu. 5 Na katika kile kiti cha enzi kunatoka umeme na sauti na ngurumo. Na taa saba za moto zilikiwaka mbele ya kile kiti cha enzi, ndizo Roho saba za Mungu. 6 Na mbele ya kile kiti cha enzi kulikuwa na mfano wa bahari ya kioo, kama bilauri; na katikati ya kile kiti cha enzi, na pande zote za kile kiti, walikuwako wenye uhai wanne, wamejaa macho mbele na nyuma. 7 Na huyo mwenye uhai wa kwanza alikuwa mfano wa simba; na mwenye uhai wa pili alikuwa mfano wa ndama; na mwenye uhai wa tatu alikuwa na uso kama uso wa mwanadamu; na mwenye uhai wa nne alikuwa mfano wa tai arukaye. 8 Na hawa wenye uhai wanne, kila mmoja alikuwa na mabawa sita; na pande zote na ndani wamejaa macho, wala hawapumziki mchana wala usiku, wakisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Bwana Mungu Mwenyezi, aliyekuwako na aliyeko na atakayekuja. 9 Na hao wenye uhai wanapompa yeye aketiye juu ya kiti cha enzi utukufu, na heshima, na shukrani, yeye aliye hai hata milele na milele, 10 ndipo hao wazee ishirini na wanne huanguka mbele zake yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi, nao humsujudia yeye aliye hai hata milele na milele, nao huzitupa taji zao mbele ya kile kiti cha enzi, wakisema, 11 Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.

Ufunuo 5

1 Kisha nikaona katika mkono wa kuume wake yeye aliyeketi juu ya kile kiti cha enzi kitabu kilichoandikwa ndani na nyuma, kimetiwa muhuri saba. 2 Nikaona malaika mwenye nguvu akihubiri kwa sauti kuu, N'nani astahiliye kukifungua kitabu, na kuzivunja muhuri zake? 3 Wala hapakuwa na mtu mbinguni, wala juu ya nchi, wala chini ya nchi, aliyeweza kukifungua hicho kitabu, wala kukitazama. 4 Nami nikalia sana kwa kuwa hapakuonekana mtu astahiliye kukifungua hicho kitabu, wala kukitazama. 5 Na mmojawapo wa wale wazee akaniambia, Usilie; tazama, Simba aliye wa kabila ya Yuda, Shina la Daudi, yeye ameshinda apate kukifungua kile kitabu, na zile muhuri zake saba. 6 Nikaona katikati ya kile kiti cha enzi na wale wenye uhai wanne, na katikati ya wale wazee, Mwana-Kondoo amesimama, alikuwa kana kwamba amechinjwa, mwenye pembe saba na macho saba, ambazo ni Roho saba za Mungu zilizotumwa katika dunia yote. 7 Akaja, akakitwaa kile kitabu katika mkono wa kuume wake yeye aliyeketi juu ya kile kiti cha enzi. 8 Hata alipokitwaa kile kitabu, hao wenye uhai wanne na wale wazee ishirini na wanne wakaanguka mbele za Mwana-Kondoo, kila mmoja wao ana kinubi, na vitasa vya dhahabu vilivyojaa manukato, ambayo ni maombi ya watakatifu. 9 Nao waimba wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, 10 ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi. 11 Nikaona nikasikia sauti ya malaika wengi pande zote za kile kiti cha enzi, na za wale wenye uhai, na za wale wazee, na hesabu yao ilikuwa elfu kumi mara elfu kumi na elfu mara elfu, 12 wakisema kwa sauti kuu, Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka. 13 Na kila kiumbe kilichoko mbinguni na juu ya nchi na chini ya nchi ya juu ya bahari, na vitu vyote vilivyomo ndani yake, nalivisikia, vikisema, Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwana-Kondoo, hata milele na milele. 14 Na wale wenye uhai wanne wakasema, Amina. Na wale wazee wakaanguka, wakasujudu.

Ufunuo 6

1Kisha nikaona napo Mwana-Kondoo alipofungua moja ya zile muhuri saba, nikasikia mmoja wa wale wenye uhai wanne akisema, kama kwa sauti ya ngurumo, Njoo! 2 Nikaona, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda ana uta, akapewa taji, naye akatoka, ali akishinda tena apate kushinda. 3 Na alipoifungua muhuri ya pili, nikamsikia yule mwenye uhai wa pili akisema, Njoo! 4 Akatoka farasi mwingine, mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa. 5 Na alipoifungua muhuri ya tatu, nikamsikia yule wa tatu mwenye uhai akisema, Njoo! Nikaona, na tazama, farasi mweusi, na yeye aliyempanda ana mizani mkononi mwake. 6 Nikasikia kama sauti katikati ya hao wenye uhai wanne, ikisema, Kibaba cha ngano kwa nusu rupia, na vibaba vitatu vya shayiri kwa nusu rupia, wala usiyadhuru mafuta wala divai. 7 Na alipoifungua muhuri ya nne, nikasikia sauti ya yule mwenye uhai wa nne akisema, Njoo! 8 Nikaona, na tazama, farasi wa rangi ya kijivujivu, na yeye aliyempanda jina lake ni Mauti, na Kuzimu akafuatana naye. Nao wakapewa mamlaka juu ya robo ya nchi, waue kwa upanga na kwa njaa na kwa tauni na kwa hayawani wa nchi. 9 Na alipoifungua muhuri ya tano, nikaona chini ya madhabahu roho zao waliochinjwa kwa ajili ya neno la Mungu, na kwa ajili ya ushuhuda waliokuwa nao. 10 Wakalia kwa sauti kuu, wakisema, Ee Mola, Mtakatifu, Mwenye kweli, hata lini kutokuhukumu, wala kuipatia haki damu yetu kwa hao wakaao juu ya nchi? 11 Nao wakapewa kila mmoja nguo ndefu, nyeupe, wakaambiwa wastarehe bado muda mchache, hata itakapotimia hesabu ya wajoli wao na ndugu zao, watakaouawa vile vile kama wao. 12 Nami nikaona, alipoifungua muhuri ya sita, palikuwa na tetemeko kuu la nchi; jua likawa jeusi kama gunia la singa, mwezi wote ukawa kama damu, 13 na nyota zikaanguka juu ya nchi kama vile mtini upukutishavyo mapooza yake, utikiswapo na upepo mwingi. 14 Mbingu zikaondolewa kama ukurasa ulivyokunjwa, na kila mlima na kisiwa kikahamishwa kutoka mahali pake. 15 Na wafalme wa dunia, na wakuu, na majemadari, na matajiri, na wenye nguvu, na kila mtumwa, na mwungwana, wakajificha katika pango na chini ya miamba ya milima, 16 wakiiambia milima na miamba, Tuangukieni, tusitirini, mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na hasira ya Mwana-Kondoo. 17 Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama?

Ufunuo 7

1 Baada ya hayo nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wo wote. 2 Nikaona malaika mwingine, akipanda kutoka maawio ya jua, mwenye muhuri ya Mungu aliye hai; akawapigia kelele kwa sauti kuu wale malaika wanne waliopewa kuidhuru nchi na bahari, 3 akisema, Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao. 4 Nikasikia hesabu yao waliotiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli, watu mia na arobaini na nne elfu. 5 Wa kabila ya Yuda kumi na mbili elfu waliotiwa muhuri. Wa kabila ya Reubeni kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Gadi kumi na mbili elfu. 6 Wa kabila ya Asheri kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Naftali kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Manase kumi na mbili elfu. 7 Wa kabila ya Simeoni kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Lawi kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Isakari kumi na mbili elfu. 8 Wa kabila ya Zabuloni kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Yusufu kumi na mbili elfu. Wa kabila ya Benyamini kumi na mbili elfu waliotiwa muhuri. 9 Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; 10 wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo. 11 Na malaika wote walikuwa wakisimama pande zote za kile kiti cha enzi, na za hao wazee, na za wale wenye uhai wanne, nao wakaanguka kifulifuli mbele ya kile kiti cha enzi, wakamsujudu Mungu, 12 wakisema, Amina; Baraka na utukufu na hekima na shukrani na heshima na uweza na nguvu zina Mungu wetu hata milele na milele. Amina. 13 Akajibu mmoja wa wale wazee akiniambia, Je! Watu hawa waliovikwa mavazi meupe ni akina nani? Na wametoka wapi? 14 Nikamwambia, Bwana wangu, wajua wewe. Akaniambia, Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. 15 Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake, na yeye aketiye katika kiti cha enzi atatanda hema yake juu yao. 16 Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena, wala jua halitawapiga, wala hari iliyo yote. 17 Kwa maana huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.

Ufunuo 8

1 Hata alipoifungua muhuri ya saba, kukawa kimya mbinguni kama muda wa nusu saa. 2 Nami nikawaona wale malaika saba wasimamao mbele za Mungu, nao wakapewa baragumu saba. 3 Na malaika mwingine akaja akasimama mbele ya madhabahu, mwenye chetezo cha dhahabu, akapewa uvumba mwingi, ili autie pamoja na maombi ya watakatifu wote juu ya madhabahu ya dhahabu, iliyo mbele ya kiti cha enzi. 4 Na moshi wa ule uvumba ukapanda mbele za Mungu pamoja na maombi ya watakatifu, kutoka mkononi mwa malaika. 5 Na huyo malaika akakitwaa kile chetezo, akakijaza moto wa madhabahu, akautupa juu ya nchi, kukawa radi na sauti na umeme na tetemeko la nchi. 6 Na wale malaika saba wenye baragumu saba wakajifanya tayari ili wazipige. 7 Malaika wa kwanza akapiga baragumu, kukawa mvua ya mawe na moto vilivyotangamana na damu, vikatupwa juu ya nchi; theluthi ya nchi ikateketea, na theluthi ya miti ikateketea, na majani mabichi yote yakateketea. 8 Malaika wa pili akapiga baragumu, na kitu, mfano wa mlima mkubwa uwakao moto, kikatupwa katika bahari; theluthi ya bahari ikawa damu. 9 Wakafa theluthi ya viumbe vilivyomo baharini, vyenye uhai; theluthi ya merikebu zikaharibiwa. 10 Malaika wa tatu akapiga baragumu, nyota kubwa ikaanguka kutoka mbinguni, iliyokuwa ikiwaka kama taa, ikaanguka juu ya theluthi ya mito, na juu ya chemchemi za maji. 11 Na jina lake ile nyota yaitwa Pakanga; theluthi ya maji ikawa pakanga, na wanadamu wengi wakafa kwa maji hayo, kwa kuwa yalitiwa uchungu. 12 Malaika wa nne akapiga baragumu, theluthi ya jua ikapigwa, na theluthi ya mwezi, na theluthi ya nyota, ili kwamba ile theluthi itiwe giza, mchana usiangaze theluthi yake, wala usiku vivyo hivyo. 13 Kisha nikaona, nikasikia tai mmoja akiruka katikati ya mbingu, akisema kwa sauti kuu, Ole, ole, ole wao wakaao juu ya nchi! Kwa sababu ya sauti zisaliazo za baragumu za malaika watatu, walio tayari kupiga.

Ufunuo 9

1 Malaika wa tano akapiga baragumu, nikaona nyota iliyotoka mbinguni, imeanguka juu ya nchi; naye akapewa ufunguo wa shimo la kuzimu. 2 Akalifungua shimo la kuzimu; moshi ukapanda kutoka mle shimoni kama moshi wa tanuru kubwa; jua na anga vikatiwa giza kwa sababu ya ule moshi wa shimoni. 3 Nzige wakatoka katika ule moshi, wakaenda juu ya nchi, wakapewa nguvu kama nguvu waliyo nayo nge wa nchi. 4 Wakaambiwa wasiyadhuru majani ya nchi, wala kitu cho chote kilicho kibichi, wala mti wo wote, ila wale watu wasio na muhuri ya Mungu katika vipaji vya nyuso zao. 5 Wakapewa amri kwamba wasiwaue, bali wateswe miezi mitano. Na maumivu yao yalikuwa kama kuumwa na nge, aumapo mwanadamu. 6 Na siku zile wanadamu watatafuta mauti, wala hawataiona kamwe. Nao watatamani kufa, nayo mauti itawakimbia. 7 Na maumbo ya hao nzige yalikuwa kama farasi waliowekwa tayari kwa vita, na juu ya vichwa vyao kama taji, mfano wa dhahabu, na nyuso zao zilikuwa kama nyuso za wanadamu. 8 Nao walikuwa na nywele kama nywele za wanawake. Na meno yao yalikuwa kama meno ya simba. 9 Nao walikuwa na dirii kifuani kama dirii za chuma. Na sauti ya mabawa yao ilikuwa kama sauti ya magari, ya farasi wengi waendao kasi vitani. 10 Nao wana mikia kama ya nge, na miiba; na nguvu yao ya kuwadhuru wanadamu miezi mitano ilikuwa katika mikia yao. 11 Na juu yao wanaye mfalme, naye ni malaika wa kuzimu, jina lake kwa Kiebrania ni Abadoni, na kwa Kiyunani analo jina lake Apolioni. 12 Ole wa kwanza umekwisha pita. Tazama, bado ziko ole mbili, zinakuja baadaye. 13 Malaika wa sita akapiga baragumu, nikasikia sauti moja iliyotoka katika zile pembe za madhabahu ya dhahabu iliyo mbele za Mungu, 14 ikimwambia yule malaika wa sita aliyekuwa na baragumu, Wafungue nao malaika wanne waliofungwa kwenye mto mkubwa Frati. 15 Wale malaika wanne wakafunguliwa, waliokuwa wamewekwa tayari kwa ile saa na siku na mwezi na mwaka, ili kwamba waue theluthi ya wanadamu. 16 Na hesabu ya majeshi ya wapanda farasi ilikuwa elfu ishirini mara elfu kumi; nilisikia hesabu yao. 17 Hiyo ndivyo nilivyowaona hao farasi katika maono yangu, nao waliokaa juu yao, wana dirii kifuani, kama za moto, na za samawi, na za kiberiti; na vichwa vya farasi hao ni kama vichwa vya simba, na katika vinywa vyao hutoka moto na moshi na kiberiti. 18 Theluthi ya wanadamu wakauawa kwa mapigo matatu hayo, kwa moto huo na moshi huo na kiberiti hicho, yaliyotoka katika vinywa vyao. 19 Kwa maana nguvu za hao farasi ni katika vinywa vyao, na katika mikia yao; maana mikia yao ni mfano wa nyoka, ina vichwa, nao wanadhuru kwa hivyo. 20 Na wanadamu waliosalia, wasiouawa kwa mapigo hayo, hawakuzitubia zile kazi za mikono yao, hata wasiwasujudie mashetani, na sanamu za dhahabu na za fedha na za shaba na za mawe na za miti, zisizoweza kuona wala kusikia wala kuenenda. 21 Wala hawakuutubia uuaji wao, wala uchawi wao, wala uasherati wao, wala wivi wao.

Ufunuo 10

1 Kisha nikaona malaika mwingine mwenye nguvu akishuka kutoka mbinguni, amevikwa wingu; na upinde wa mvua juu ya kichwa chake; na uso wake ulikuwa kama jua, na miguu yake kama nguzo za moto. 2 Na katika mkono wake alikuwa na kitabu kidogo kimefunguliwa. Akaweka mguu wake wa kuume juu ya bahari, nao wa kushoto juu ya nchi. 3 Naye akalia kwa sauti kuu, kama simba angurumavyo. Na alipolia, zile ngurumo saba zikatoa sauti zao. 4 Hata ngurumo saba zilipotoa sauti zao, nalikuwa tayari kuandika. Nami nalisikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Yatie muhuri maneno hayo yaliyonenwa na hizo ngurumo saba, usiyaandike. 5 Na yule malaika niliyemwona, akisimama juu ya bahari na juu ya nchi, akainua mkono wake wa kuume kuelekea mbinguni, 6 akaapa kwa yeye aliye hai hata milele na milele, yeye aliyeziumba mbingu na vitu vilivyomo, na nchi na vitu vilivyomo, na bahari na vitu vilivyomo, ya kwamba hapatakuwa na wakati baada ya haya; 7 isipokuwa katika siku za sauti ya malaika wa saba atakapokuwa tayari kupiga baragumu; hapo ndipo siri ya Mungu itakapotimizwa, kama alivyowahubiri watumishi wake hao manabii. 8 Na sauti ile niliyoisikia kutoka mbinguni ilinena nami tena, ikisema, Enenda, ukakitwae kile kitabu kilichofunguliwa katika mkono wa yule malaika, aliyesimama juu ya bahari na juu ya nchi. 9 Nikamwendea malaika yule nikamwambia kwamba anipe kile kitabu kidogo. Akaniambia, Kitwae, ukile, nacho kitakutia uchungu tumboni mwako, bali katika kinywa chako kitakuwa kitamu kama asali. 10 Nikakitwaa kile kitabu kidogo katika mkono wa malaika yule, nikakila; nacho kikawa kitamu kama asali kinywani mwangu, na nilipokwisha kukila tumbo langu likatiwa uchungu. 11 Wakaniambia, Imekupasa kutoa unabii tena juu ya watu na taifa na lugha na wafalme wengi.

Ufunuo 11

1 Nikapewa mwanzi kama fimbo; na mmoja akaniambia, Inuka, ukalipime hekalu la Mungu, na madhabahu, na hao wasujuduo humo. 2 Na behewa iliyo nje ya hekalu uiache nje wala usiipime, kwa maana Mataifa wamepewa hiyo, nao wataukanyaga mji mtakatifu miezi arobaini na miwili. 3 Nami nitawaruhusu mashahidi wangu wawili, nao watatoa unabii siku elfu na mia mbili na sitini, hali wamevikwa magunia. 4 Hao ndio ile mizeituni miwili na vile vinara viwili visimamavyo mbele za Bwana wa nchi. 5 Na mtu akitaka kuwadhuru, moto hutoka katika vinywa vyao na kuwala adui zao. Na mtu akitaka kuwadhuru, hivyo ndivyo impasavyo kuuawa. 6 Hao wana amri ya kuzifunga mbingu, ili mvua isinyeshe katika siku za unabii wao. Nao wana amri juu ya maji kuyageuza kuwa damu, na kuipiga nchi kwa kila pigo, kila watakapo. 7 Hata watakapoumaliza ushuhuda wao, yule mnyama atokaye katika kuzimu atafanya vita nao, naye atawashinda na kuwaua. 8 Na mizoga yao itakuwa katika njia ya mji ule mkuu, uitwao kwa jinsi ya roho Sodoma, na Misri, tena ni hapo Bwana wao aliposulibiwa. 9 Na watu wa hao jamaa na kabila na lugha na taifa waitazama mizoga yao siku tatu u nusu, wala hawaiachi mizoga yao kuwekwa kaburini. 10 Nao wakaao juu ya nchi wafurahi juu yao na kushangilia. Nao watapelekeana zawadi wao kwa wao, kwa kuwa manabii hao wawili waliwatesa wao wakaao juu ya nchi. 11 Na baada ya siku hizo tatu u nusu, roho ya uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu kuu ikawaangukia watu waliowatazama. 12 Wakasikia sauti kuu kutoka mbinguni ikiwaambia, Pandeni hata huku. Wakapanda mbinguni katika wingu, adui zao wakiwatazama. 13 Na katika saa ile palikuwa na tetemeko kuu la nchi, na sehemu ya kumi ya mji ikaanguka; wanadamu elfu saba wakauawa katika tetemeko lile. Na waliosalia wakaingiwa na hofu, wakamtukuza Mungu wa mbingu. 14 Ole wa pili umekwisha pita, tazama ole wa tatu unakuja upesi. 15 Malaika wa saba akapiga baragumu, pakawa na sauti kuu katika mbingu, zikisema, Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele. 16 Na wale wazee ishirini na wanne waketio mbele za Mungu katika viti vya enzi vyao wakaanguka kifulifuli, wakamsujudia Mungu 17 wakisema, Tunakushukuru wewe, Bwana Mungu Mwenyezi, uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu umeutwaa uweza wako ulio mkuu, na kumiliki. 18 Na mataifa walikasirika, hasira yako nayo ikaja, na wakati ukaja wa kuhukumiwa waliokufa, na wa kuwapa thawabu yao watumwa wako manabii na watakatifu, na hao walichao jina lako, wadogo kwa wakubwa, na wa kuwaharibu hao waiharibuo nchi. 19 Kisha Hekalu la Mungu lililoko mbinguni likafunguliwa, na sanduku la agano lake likaonekana ndani ya hekalu lake. Kukawa na umeme, na sauti, na radi, na tetemeko la nchi, na mvua ya mawe nyingi sana.

Ufunuo 12

1 Na ishara kuu ilionekana mbinguni; mwanamke aliyevikwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu yake, na juu ya kichwa chake taji ya nyota kumi na mbili. 2 Naye alikuwa ana mimba, akilia, hali ana utungu na kuumwa katika kuzaa. 3 Ikaonekana ishara nyingine mbinguni; na tazama, joka kubwa jekundu, alikuwa na vichwa saba na pembe kumi, na juu ya vichwa vyake vilemba saba. 4 Na mkia wake wakokota theluthi ya nyota za mbinguni, na kuziangusha katika nchi. Na yule joka akasimama mbele ya yule mwanamke aliye tayari kuzaa, ili azaapo, amle mtoto wake. 5 Naye akazaa mtoto mwanamume, yeye atakayewachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Na mtoto wake akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti chake cha enzi. 6 Yule mwanamke akakimbilia nyikani, ambapo ana mahali palipotengenezwa na Mungu, ili wamlishe huko muda wa siku elfu na mia mbili na sitini. 7 Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; 8 nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. 9 Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye. 10 Nikasikia sauti kuu mbinguni, ikisema, Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. 11 Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa. 12 Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! Kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu. 13 Na joka yule alipoona ya kuwa ametupwa katika nchi, alimwudhi mwanamke yule aliyemzaa mtoto mwanamume. 14 Mwanamke yule akapewa mabawa mawili ya tai yule mkubwa, ili aruke, aende zake nyikani hata mahali pake, hapo alishwapo kwa wakati na nyakati na nusu ya wakati, mbali na nyoka huyo. 15 Nyoka akatoa katika kinywa chake, nyuma ya huyo mwanamke, maji kama mto, amfanye kuchukuliwa na mto ule. 16 Nchi ikamsaidia mwanamke; nchi ikafunua kinywa chake, ikaumeza mto ule alioutoa yule joka katika kinywa chake. 17 Joka akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu; naye akasimama juu ya mchanga wa bahari.

Ufunuo 13

1 Kisha nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba, na juu ya pembe zake ana vilemba kumi, na juu ya vichwa vyake majina ya makufuru. 2 Na yule mnyama niliyemwona alikuwa mfano wa chui, na miguu yake ilikuwa kama miguu ya dubu, na kinywa chake kama kinywa cha simba, yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi. 3 Nikaona kimoja cha vichwa vyake kana kwamba kimetiwa jeraha la mauti, na pigo lake la mauti likapona. Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule. 4 Wakamsujudu yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye? 5 Naye akapewa kinywa cha kunena maneno makuu, ya makufuru. Akapewa uwezo wa kufanya kazi yake miezi arobaini na miwili. 6 Akafunua kinywa chake amtukane Mungu, na kulitukana jina lake, na maskani yake, nao wakaao mbinguni. 7 Tena akapewa kufanya vita na watakatifu na kuwashinda, akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa. 8 Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo, aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia. 9 Mtu akiwa na sikio na asikie. 10 Mtu akichukua mateka, atachukuliwa mateka. Mtu akiua kwa upanga, atauawa kwa upanga. Hapa ndipo penye subira na imani ya watakatifu. 11 Kisha nikaona mnyama mwingine, akipanda juu kutoka katika nchi; naye alikuwa na pembe mbili mfano wa Mwana-Kondoo, akanena kama joka. 12 Naye atumia uwezo wote wa mnyama yule wa kwanza mbele yake. Naye aifanya dunia na wote wakaao ndani yake wamsujudie mnyama wa kwanza, ambaye jeraha lake la mauti lilipona. 13 Naye afanya ishara kubwa, hata kufanya moto kushuka kutoka mbinguni uje juu ya nchi mbele ya wanadamu. 14 Naye awakosesha wale wakaao juu ya nchi, kwa ishara zile alizopewa kuzifanya mbele ya huyo mnyama, akiwaambia wakaao juu ya nchi kumfanyia sanamu yule mnyama, aliyekuwa na jeraha la upanga naye akaishi. 15 Akapewa kutia pumzi katika ile sanamu ya mnyama, hata ile sanamu ya mnyama inene, na kuwafanya hao wote wasioisujudu sanamu ya mnyama wauawe. 16 Naye awafanya wote, wadogo kwa wakubwa, na matajiri kwa maskini, na walio huru kwa watumwa, watiwe chapa katika mkono wao wa kuume, au katika vipaji vya nyuso zao; 17 tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake. 18 Hapa ndipo penye hekima. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita.

Ufunuo 14

1 Kisha nikaona, na tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao. 2 Nami nikasikia sauti kutoka mbinguni, kama sauti ya maji mengi, na kama sauti ya radi kuu. Na hiyo sauti niliyoisikia ilikuwa kama sauti ya wapiga vinubi, wakivipiga vinubi vyao; 3 na kuimba wimbo mpya mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele ya wale wenye uhai wanne, na wale wazee; wala hapana mtu aliyeweza kujifunza wimbo ule, ila wale mia na arobaini na nne elfu, walionunuliwa katika nchi. 4 Hawa ndio wasiotiwa unajisi pamoja na wanawake, kwa maana ni bikira. Hawa ndio wamfuatao Mwana-Kondoo kila aendako. Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. 5 Na katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa. 6 Kisha nikaona malaika mwingine, akiruka katikati ya mbingu, mwenye Injili ya milele, awahubiri hao wakaao juu ya nchi, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa, 7 akasema kwa sauti kuu, Mcheni Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja. Msujudieni yeye aliyezifanya mbingu na nchi na bahari na chemchemi za maji. 8 Kisha mwingine, malaika wa pili, akafuata, akisema, Umeanguka, umeanguka Babeli, mji ule ulio mkubwa, maana ndio uliowanywesha mataifa yote mvinyo ya ghadhabu ya uasherati wake. 9 Na mwingine, malaika wa tatu, akawafuata, akisema kwa sauti kuu, Mtu awaye yote akimsujudu huyo mnyama na sanamu yake, na kuipokea chapa katika kipaji cha uso wake, au katika mkono wake, 10 yeye naye atakunywa katika mvinyo ya ghadhabu ya Mungu iliyotengenezwa, pasipo kuchanganywa na maji, katika kikombe cha hasira yake; naye atateswa kwa moto na kiberiti mbele ya malaika watakatifu, na mbele za Mwana-Kondoo. 11 Na moshi wa maumivu yao hupanda juu hata milele na milele, wala hawana raha mchana wala usiku, hao wamsujuduo huyo mnyama na sanamu yake, na kila aipokeaye chapa ya jina lake. 12 Hapa ndipo penye subira ya watakatifu, hao wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu. 13 Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Andika, Heri wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, asema Roho, wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao. 14 Kisha nikaona, na tazama, wingu jeupe, na juu ya wingu hilo ameketi mmoja, mfano wa Mwanadamu, mwenye taji ya dhahabu juu ya kichwa chake, na katika mkono wake mundu mkali. 15 Na malaika mwingine akatoka katika hekalu, akimlilia kwa sauti kuu yeye aliyekuwa ameketi juu ya lile wingu, Tia mundu wako, ukavune; kwa kuwa saa ya kuvuna imekuja; kwa kuwa mavuno ya nchi yamekomaa. 16 Na yeye aliyeketi juu ya wingu akautupa mundu wake juu ya nchi, nchi ikavunwa. 17 Kisha malaika mwingine akatoka katika lile hekalu lililoko mbinguni, yeye naye ana mundu mkali. 18 Na malaika mwingine akatoka katika ile madhabahu, yule mwenye mamlaka juu ya moto; naye akamlilia kwa sauti kuu yule mwenye mundu ule mkali, akisema, Tia mundu wako mkali, ukachume vichala vya mzabibu wa nchi, maana zabibu zake zimeiva sana. 19 Malaika yule akautupa mundu wake hata nchi, akauchuma mzabibu wa nchi, akazitupa zabibu katika shinikizo hilo kubwa la ghadhabu ya Mungu. 20 Shinikizo lile likakanyagwa nje ya mji, damu ikatoka katika shinikizo mpaka kwenye hatamu za farasi, kama mwendo wa maili mia mbili.

Ufunuo 15

1 Kisha nikaona ishara nyingine katika mbingu, iliyo kubwa, na ya ajabu; malaika saba wenye mapigo saba ya mwisho; maana katika hayo ghadhabu ya Mungu imetimia. 2 Tena nikaona kitu kama mfano wa bahari ya kioo iliyochangamana na moto, na wale wenye kushinda, watokao kwa yule mnyama, na sanamu yake, na kwa hesabu ya jina lake, walikuwa wamesimama kando-kando ya hiyo bahari ya kioo, wenye vinubi vya Mungu. 3 Nao wauimba wimbo wa Musa, mtumwa wa Mungu, na wimbo wa Mwana-Kondoo, wakisema, Ni makuu, na ya ajabu, matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa. 4 Ni nani asiyekucha, Ee Bwana, na kulitukuza jina lako? Kwa kuwa wewe peke yako u Mtakatifu; kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa kuwa matendo yako ya haki yamekwisha kufunuliwa. 5 Na baada ya hayo nikaona, na hekalu la hema ya ushuhuda mbinguni lilifunguliwa; 6 na wale malaika saba, wenye mapigo saba, wakatoka katika hekalu, wamevikwa mavazi ya kitani safi, ya kung'aa, wamefungwa vifuani mwao mishipi ya dhahabu. 7 Na mmoja wa wale wenye uhai wanne akawapa wale malaika saba vitasa saba vya dhahabu, vimejaa ghadhabu ya Mungu, aliye hai hata milele na milele. 8 Hekalu likajazwa moshi uliotoka kwenye utukufu wa Mungu na uweza wake. Wala hapakuwa na mtu aliyeweza kuingia ndani ya hekalu, hata yatimizwe mapigo saba ya wale malaika saba.

Ufunuo 16

1 Nikasikia sauti kuu kutoka hekaluni, ikiwaambia wale malaika saba, Enendeni, mkavimimine vile vitasa saba vya ghadhabu ya Mungu juu ya nchi. 2 Akaenda huyo wa kwanza, akakimimina kitasa chake juu ya nchi; pakawa na jipu baya, bovu, juu ya wale watu wenye chapa ya huyo mnyama, na wale wenye kuisujudia sanamu yake. 3 Na huyo wa pili akakimimina kitasa chake juu ya bahari, ikawa damu kama damu ya mfu, na vitu vyote vyenye roho ya uhai katika bahari vikafa. 4 Na huyo wa tatu akakimimina kitasa chake juu ya mito na chemchemi za maji; zikawa damu. 5 Nami nikamsikia malaika wa maji akisema, Wewe u mwenye haki, uliyeko na uliyekuwako, Mtakatifu, kwa kuwa umehukumu hivi; 6 kwa kuwa walimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wainywe; nao wamestahili. 7 Nikaisikia hiyo madhabahu ikisema, Naam, Bwana Mungu Mwenyezi, ni za kweli, na za haki, hukumu zako. 8 Na huyo wa nne akakimimina kitasa chake juu ya jua, nalo likapewa kuwaunguza wanadamu kwa moto. 9 Wanadamu wakaunguzwa maunguzo makubwa, nao wakalitukana jina la Mungu aliye na mamlaka juu ya mapigo hayo; wala hawakutubu wala kumpa utukufu. 10 Na huyo wa tano akakimimina kitasa chake juu ya kiti cha enzi cha yule mnyama; ufalme wake ukatiwa giza; wakatafuna ndimi zao kwa sababu ya maumivu, 11 wakamtukana Mungu wa mbingu kwa sababu ya maumivu yao, na kwa sababu ya majipu yao; wala hawakuyatubia matendo yao. 12 Na huyo wa sita akakimimina kitasa chake juu ya mto ule mkubwa Frati; maji yake yakakauka, ili njia itengenezwe kwa wafalme watokao katika maawio ya jua. 13 Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka, na katika kinywa cha yule mnyama, na katika kinywa cha yule nabii wa uongo. 14 Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi. 15 (Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake.) 16 Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har-Magedoni. 17 Na huyo wa saba akakimimina kitasa chake juu ya anga. Sauti kuu ikatoka katika hekalu, katika kile kiti cha enzi, ikisema, Imekwisha kuwa. 18 Pakawa na umeme na sauti na radi; na palikuwa na tetemeko la nchi kubwa, ambalo tangu wanadamu kuwako juu ya nchi hapakuwa namna ile, jinsi lilivyokuwa kubwa tetemeko hilo. 19 Na mji ule mkuu ukagawanyikana mafungu matatu, na miji ya mataifa ikaanguka; na Babeli ule mkuu ukakumbukwa mbele za Mungu, kupewa kikombe cha mvinyo ya ghadhabu ya hasira yake. 20 Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena. 21 Na mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta, ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno.

Ufunuo 17

1 Akaja mmoja wa wale malaika saba, wenye vile vitasa saba, akanena nami, akisema, Njoo huku, nitakuonyesha hukumu ya yule kahaba mkuu aketiye juu ya maji mengi; 2 ambaye wafalme wa nchi wamezini naye, nao wakaao katika nchi wamelevywa kwa mvinyo ya uasherati wake. 3 Akanichukua katika Roho hata jangwani, nikaona mwanamke, ameketi juu ya mnyama mwekundu sana, mwenye kujaa majina ya makufuru, mwenye vichwa saba na pembe kumi. 4 Na mwanamke yule alikuwa amevikwa nguo ya rangi ya zambarau, na nyekundu, amepambwa kwa dhahabu, na kito cha thamani, na lulu, naye alikuwa na kikombe cha dhahabu mkononi mwake, kilichojawa na machukizo, na machafu ya uasherati wake. 5 Na katika kipaji cha uso wake alikuwa na jina limeandikwa, la siri, BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI. 6 Nikamwona yule mwanamke amelewa kwa damu ya watakatifu, na kwa damu ya mashahidi wa Yesu. Nami nilipomwona nikastaajabu ajabu kuu. 7 Na yule malaika akaniambia, Kwani kustaajabu? Nitakuambia siri ya mwanamke huyu, na ya mnyama huyu amchukuaye, mwenye vile vichwa saba na zile pembe kumi. 8 Yule mnyama uliyemwona alikuwako, naye hayuko, naye yu tayari kupanda kutoka kuzimu na kwenda kwenye uharibifu. Na hao wakaao juu ya nchi, wasioandikwa majina yao katika kitabu cha uzima tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu, watastaajabu wamwonapo yule mnyama, ya kwamba alikuwako, naye hayuko, naye atakuwako. 9 Hapo ndipo penye akili zenye hekima. Vile vichwa saba ni milima saba anayokalia mwanamke huyo. 10 Navyo ni wafalme saba. Watano wamekwisha kuanguka, na mmoja yupo, na mwingine hajaja bado. Naye atakapokuja imempasa kukaa muda mchache. 11 Na yule mnyama aliyekuwako naye hayuko, yeye ndiye wa nane, naye ni mmoja wa wale saba, naye aenenda kwenye uharibifu. 12 Na zile pembe kumi ulizoziona ni wafalme kumi, ambao hawajapokea ufalme bado, lakini wapokea mamlaka kama wafalme muda wa saa moja pamoja na yule mnyama. 13 Hawa wana shauri moja, nao wampa yule mnyama nguvu zao na mamlaka yao. 14 Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme, na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu. 15 Kisha akaniambia, Yale maji uliyoyaona, hapo aketipo yule kahaba, ni jamaa na makutano na mataifa na lugha. 16 Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto. 17 Maana Mungu ametia mioyoni mwao kufanya shauri lake, na kufanya shauri moja, na kumpa yule mnyama ufalme wao hata maneno ya Mungu yatimizwe. 18 Na yule mwanamke uliyemwona, ni mji ule mkubwa, wenye ufalme juu ya wafalme wa nchi.

Ufunuo 18

1 Baada ya hayo naliona malaika mwingine, akishuka kutoka mbinguni, mwenye mamlaka kuu; na nchi ikaangazwa kwa utukufu wake. 2 Akalia kwa sauti kuu, akisema, Umeanguka, umeanguka Babeli ule mkuu; umekuwa maskani ya mashetani, na ngome ya kila roho mchafu, na ngome ya kila ndege mchafu mwenye kuchukiza; 3 kwa kuwa mataifa yote wamekunywa mvinyo ya ghadhabu ya uasherati wake, na wafalme wa nchi wamezini naye, na wafanya biashara wa nchi wamepata mali kwa nguvu za kiburi chake. 4 Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni, ikisema, Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. 5 Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake. 6 Mlipeni kama yeye alivyolipa, mkamlipe mara mbili kwa kadiri ya matendo yake. Katika kikombe kile alichokichanganyisha, mchanganyishieni maradufu. 7 Kwa kadiri alivyojitukuza na kufanya anasa, mpeni maumivu na huzuni kadiri iyo hiyo. Kwa kuwa husema moyoni mwake, Nimeketi malkia, wala si mjane, wala sitaona huzuni kamwe. 8 Kwa sababu hiyo mapigo yake yatakuja katika siku moja, mauti, na huzuni, na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana Bwana Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu. 9 Na hao wafalme wa nchi, waliozini naye na kufanya anasa pamoja naye, watalia na kumwombolezea; wauonapo moshi wa kuungua kwake; 10 wakisimama mbali kwa hofu ya maumivu yake, wakisema, Ole, ole, mji ule ulio mkuu, Babeli, mji ule ulio na nguvu! Kwa kuwa katika saa moja hukumu yako imekuja. 11 Nao wafanya biashara wa nchi walia na kumwombolezea, kwa sababu hapana mtu anunuaye bidhaa yao tena; 12 bidhaa ya dhahabu, na fedha, na kito chenye thamani, na lulu, na kitani nzuri, na nguo ya rangi ya zambarau, na hariri, na nguo nyekundu; na kila mti wa uudi, na kila chombo cha pembe, na kila chombo cha mti wa thamani nyingi, na cha shaba, na cha chuma, na cha marimari; 13 na mdalasini, na iliki, na uvumba, na marhamu, na ubani, na mvinyo, na mafuta ya mzeituni, na unga mzuri, na ngano, na ng'ombe, na kondoo, na farasi, na magari, na miili na roho za wanadamu. 14 Na matunda yaliyotamaniwa na roho yako yamekuondokea; na vitu vyote vilivyo laini na vitu vya fahari vimekupotea; wala watu hawataviona tena kamwe. 15 Na wafanya biashara ya vitu hivyo, waliopata mali kwake, watasimama mbali, kwa hofu ya maumivu yake; wakilia na kuomboleza, 16 wakisema, Ole, ole, mji ule mkuu! Uliovikwa kitani nzuri, na nguo ya rangi ya zambarau, na nguo nyekundu, na kupambwa kwa dhahabu, na kito cha thamani, na lulu; 17 kwa kuwa katika saa moja utajiri mwingi namna hii umekuwa ukiwa. Na kila nahodha na kila aendaye mahali popote kwa matanga, na mabaharia, nao wote watendao kazi baharini, wakasimama mbali; 18 wakalia sana, walipouona moshi wa kuungua kwake, wakisema, Ni mji upi ulio mfano wa mji huu mkubwa! 19 Wakatupa mavumbi juu ya vichwa vyao, wakalia, wakitokwa na machozi na kuomboleza, wakisema, Ole, ole, mji ule ulio mkuu! Ambao ndani yake wote wenye merikebu baharini walipata mali kwa utajiri wake; kwa kuwa katika saa moja umekuwa ukiwa. 20 Furahini juu yake, enyi mbingu, nanyi watakatifu na mitume na manabii; kwa maana Mungu amehukumu hukumu yenu juu yake. 21 Na malaika mmoja mwenye nguvu akainua jiwe, kama jiwe kubwa la kusagia, akalitupa katika bahari, akisema, Kama hivi, kwa nguvu nyingi, utatupwa Babeli, mji ule mkuu, wala hautaonekana tena kabisa. 22 Wala sauti ya wapiga vinanda, na ya wapiga zomari, na ya wapiga filimbi, na ya wapiga baragumu, haitasikiwa ndani yako tena kabisa; wala fundi awaye yote wa kazi yo yote hataonekana ndani yako tena kabisa; wala sauti ya jiwe la kusagia haitasikiwa ndani yako tena kabisa; 23 wala nuru ya taa haitamulika ndani yako tena kabisa; wala sauti ya bwana-arusi na bibi-arusi haitasikiwa ndani yako tena kabisa; maana hao wafanya biashara wako walikuwa wakuu wa nchi, kwa kuwa mataifa yote walidanganywa kwa uchawi wako. 24 Na ndani yake ilionekana damu ya manabii, na ya watakatifu, na ya wale wote waliouawa juu ya nchi.

Ufunuo 19

1 Baada ya hayo nikasikia sauti kama sauti ya makutano mengi, sauti kubwa mbinguni, ikisema, Haleluya; wokovu na utukufu na nguvu zina BWANA MUNGU wetu. 2 kwa kuwa hukumu zake ni za kweli na za haki; maana amemhukumu yule kahaba mkuu aliyeiharibu nchi kwa uasherati wake, na kuipatiliza damu ya watumwa wake mkononi mwake. 3 Wakasema mara ya pili, Haleluya. Na moshi wake hupaa juu hata milele na milele. 4 Na wale wazee ishirini na wanne, na wale wenye uhai wanne, wakasujudu na kumwabudu Mungu, aketiye katika kile kiti cha enzi, wakisema, Amina, Haleluya. 5 Sauti ikatoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Msifuni Mungu wetu, enyi watumwa wake wote, ninyi mnaomcha, wadogo kwa wakuu. 6 Nikasikia sauti kama sauti ya makutano mengi, na kama sauti ya maji mengi, na kama sauti ya radi yenye nguvu, ikisema, Haleluya; kwa kuwa Bwana Mungu wetu, Mwenyezi, amemiliki. 7 Na tufurahi, tukashangilie, tukampe utukufu wake; kwa kuwa arusi ya Mwana-Kondoo imekuja, na mkewe amejiweka tayari. 8 Naye amepewa kuvikwa kitani nzuri, ing'arayo, safi; kwa maana kitani nzuri hiyo ni matendo ya haki ya watakatifu. 9 Naye akaniambia, Andika, Heri walioalikwa karamu ya arusi ya Mwana-Kondoo. Akaniambia, Maneno haya ni maneno ya kweli ya Mungu. 10 Nami nikaanguka mbele ya miguu yake, ili nimsujudie; akaniambia, Angalia, usifanye hivi; mimi ni mjoli wako na wa ndugu zako walio na ushuhuda wa Yesu. Msujudie Mungu. Kwa maana ushuhuda wa Yesu ndio roho ya unabii. 11 Kisha nikaziona mbingu zimefunuka, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda, aitwaye Mwaminifu na Wa-kweli, naye kwa haki ahukumu na kufanya vita. 12 Na macho yake yalikuwa kama mwali wa moto, na juu ya kichwa chake vilemba vingi; naye ana jina lililoandikwa, asilolijua mtu ila yeye mwenyewe. 13 Naye amevikwa vazi lililochovywa katika damu, na jina lake aitwa, Neno la Mungu. 14 Na majeshi yaliyo mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe, safi. 15 Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi. 16 Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA Bwana WA MABwana. 17 Kisha nikaona malaika mmoja amesimama katika jua; akalia kwa sauti kuu, akiwaambia ndege wote warukao katikati ya mbingu, Njoni mkutane kwa karamu ya Mungu iliyo kuu; 18 mpate kula nyama ya wafalme, na nyama ya majemadari, na nyama ya watu hodari, na nyama ya farasi na ya watu wawapandao, na nyama ya watu wote, waungwana kwa watumwa, wadogo kwa wakubwa. 19 Kisha nikamwona huyo mnyama, na wafalme wa nchi, na majeshi yao, wamekutana kufanya vita na yeye aketiye juu ya farasi yule, tena na majeshi yake. 20 Yule mnyama akakamatwa, na yule nabii wa uongo pamoja naye, yeye aliyezifanya hizo ishara mbele yake, ambazo kwa hizo aliwadanganya watu wale walioipokea ile chapa ya huyo mnyama, nao walioisujudia sanamu yake; hao wawili wakatupwa wangali hai katika lile ziwa la moto liwakalo kwa kiberiti; 21 na wale waliosalia waliuawa kwa upanga wake yeye aliyeketi juu ya yule farasi, upanga utokao katika kinywa chake. Na ndege wote wakashiba kwa nyama zao.

Ufunuo 20

1 Kisha nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. 2 Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; 3 akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie; na baada ya hayo yapasa afunguliwe muda mchache. 4 Kisha nikaona viti vya enzi, wakaketi juu yake, nao wakapewa hukumu; nami nikaona roho zao waliokatwa vichwa kwa ajili ya ushuhuda wa Yesu, na kwa ajili ya neno la Mungu, na hao wasiomsujudia yule mnyama, wala sanamu yake, wala hawakuipokea ile chapa katika vipaji vya nyuso zao, wala katika mikono yao; nao wakawa hai, wakatawala pamoja na Kristo miaka elfu. 5 Hao wafu waliosalia hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu. 6 Huo ndio ufufuo wa kwanza. Heri, na mtakatifu, ni yeye aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hao mauti ya pili haina nguvu; bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu. 7 Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake; 8 naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi, Gogu na Magogu, kuwakusanya kwa vita, ambao hesabu yao ni kama mchanga wa bahari. 9 Wakapanda juu ya upana wa nchi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala. 10 Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele. 11 Kisha nikaona kiti cha enzi, kikubwa, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana. 12 Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao. 13 Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake. 14 Mauti na Kuzimu zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto. 15 Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto.

Ufunuo 21

1 Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena. 2 Nami nikauona mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe. 3 Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. 4 Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita. 5 Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli. 6 Akaniambia, Imekwisha kuwa. Mimi ni Alfa na Omega, Mwanzo na Mwisho. Mimi nitampa yeye mwenye kiu, ya chemchemi ya maji ya uzima, bure. 7 Yeye ashindaye atayarithi haya, nami nitakuwa Mungu wake, naye atakuwa mwanangu. 8 Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili. 9 Akaja mmoja wa wale malaika saba waliokuwa na vile vitasa saba vilivyojaa yale mapigo saba ya mwisho, naye akanena nami, akisema, Njoo huku, nami nitakuonyesha yule Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo. 10 Akanichukua katika Roho mpaka mlima mkubwa, mrefu, akanionyesha ule mji mtakatifu, Yerusalemu, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mwenyezi Mungu; 11 wenye utukufu wa Mungu, na mwangaza wake ulikuwa mfano wa kito chenye thamani nyingi kama kito cha yaspi, safi kama bilauri; 12 ulikuwa na ukuta mkubwa, mrefu, wenye milango kumi na miwili, na katika ile milango malaika kumi na wawili; na majina yameandikwa ambayo ni majina ya kabila kumi na mbili za Waisraeli. 13 Upande wa mashariki milango mitatu; na upande wa kaskazini milango mitatu; na upande wa kusini milango mitatu; na upande wa magharibi milango mitatu. 14 Na ukuta wa mji ulikuwa na misingi kumi na miwili, na katika ile misingi majina kumi na mawili ya wale mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo. 15 Na yeye aliyesema nami alikuwa na mwanzi wa dhahabu, apate kuupima huo mji, na milango yake, na ukuta wake. 16 Na ule mji ni wa mraba, na marefu yake sawasawa na mapana yake. Akaupima mji kwa ule mwanzi; ulikuwa kama maili elfu na mia tano; marefu yake na mapana yake na kwenda juu kwake ni sawasawa. 17 Akaupima ukuta wake, ukapata dhiraa mia na arobaini na nne, kwa kipimo cha kibinadamu, maana yake, cha malaika. 18 Na majenzi ya ule ukuta wake yalikuwa ya yaspi, na mji ule ulikuwa wa dhahabu safi, mfano wa kioo safi. 19 Na misingi ya ukuta wa mji ilikuwa imepambwa kwa vito vya thamani vya kila namna. Msingi wa kwanza ulikuwa yaspi; wa pili yakuti samawi; wa tatu kalkedoni; wa nne zumaridi; 20 wa tano sardoniki; wa sita akiki; wa saba krisolitho; wa nane zabarajadi; wa kenda yakuti ya manjano; wa kumi krisopraso; wa kumi na moja hiakintho; wa kumi na mbili amethisto. 21 Na ile milango kumi na miwili ni lulu kumi na mbili; kila mlango ni lulu moja. Na njia ya mji ni dhahabu safi kama kioo kiangavu. 22 Nami sikuona hekalu ndani yake; kwa maana Bwana Mungu Mwenyezi na Mwana-Kondoo, ndio hekalu lake. 23 Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo. 24 Na mataifa watatembea katika nuru yake. Na wafalme wa nchi huleta utukufu wao ndani yake. 25 Na milango yake haitafungwa kamwe mchana; kwa maana humo hamna usiku. 26 Nao wataleta utukufu na heshima ya mataifa ndani yake. 27 Na ndani yake hakitaingia kamwe cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo.

Ufunuo 22

1 Kisha akanionyesha mto wa maji ya uzima, wenye kung'aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo, 2 katikati ya njia kuu yake. Na upande huu na upande huu wa ule mto, ulikuwapo mti wa uzima, uzaao matunda, aina kumi na mbili, wenye kutoa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo ni ya kuwaponya mataifa. 3 Wala hapatakuwa na laana yo yote tena. Na kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwamo ndani yake. Na watumwa wake watamtumikia; 4 nao watamwona uso wake, na jina lake litakuwa katika vipaji vya nyuso zao. 5 Wala hapatakuwa na usiku tena; wala hawana haja ya taa wala ya nuru ya jua; kwa kuwa Bwana Mungu huwatia nuru, nao watatawala hata milele na milele. 6 Kisha akaniambia, Maneno haya ni amini na kweli. Naye Bwana, Mungu wa roho za manabii, alimtuma malaika wake kuwaonyesha watumwa wake mambo ambayo hayana budi kuwako upesi. 7 Na tazama, naja upesi; heri yeye ayashikaye maneno ya unabii wa kitabu hiki. 8 Nami Yohana ndimi niliyeyasikia na kuyaona mambo hayo. Na hapo nilipoyasikia na kuyaona nalianguka, ili nisujudu mbele ya miguu ya malaika yule mwenye kunionyesha hayo. 9 Naye akaniambia, Angalia, usifanye hivi; mimi ni mjoli wako, na wa ndugu zako manabii, na wa wale wayashikao maneno ya kitabu hiki. Msujudie Mungu. 10 Akaniambia, Usiyatie muhuri maneno ya unabii wa kitabu hiki, kwa maana wakati huo umekaribia. 11 Mwenye kudhulumu na azidi kudhulumu; na mwenye uchafu na azidi kuwa mchafu; na mwenye haki na azidi kufanya haki; na mtakatifu na azidi kutakaswa. 12 Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo. 13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho. 14 Heri wazifuao nguo zao, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake. 15 Huko nje wako mbwa, na wachawi, na wazinzi, na wauaji, na hao waabuduo sanamu, na kila mtu apendaye uongo na kuufanya. 16 Mimi Yesu nimemtuma malaika wangu kuwashuhudia ninyi mambo hayo katika makanisa. Mimi ndimi niliye Shina na Mzao wa Daudi, ile nyota yenye kung'aa ya asubuhi. 17 Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure. 18 Namshuhudia kila mtu ayasikiaye maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mtu ye yote akiyaongeza, Mungu atamwongezea hayo mapigo yaliyoandikwa katika kitabu hiki. 19 Na mtu ye yote akiondoa lo lote katika maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mungu atamwondolea sehemu yake katika ule mti wa uzima, na katika ule mji mtakatifu, ambao habari zake zimeandikwa katika kitabu hiki. 20 Yeye mwenye kuyashuhudia haya asema, Naam; naja upesi. Amina; na uje, Bwana Yesu. 21 Neema ya Bwana Yesu na iwe pamoja nanyi nyote. Amina.